Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Dr. Christina Christopher Mnzava (42 total)

MHE. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu yenye matumaini kutoka kwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kabla sijauliza, napenda kuwashukuru wananchi wa Mkoa wa Shinyanga hasa wanawake walioweza kunichagua na chama changu kuniteua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza la nyongeza; kwa kuwa ili hospitali iweze kukamilika na kuanza kufanya kazi ni lazima miundombinu yote iwepo kama maabara, X-Ray na mortuary. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba majengo mengine na miundombinu mingine inakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa tumeanza kuona jitihada nzuri za Wizara ya Afya katika kudhibiti wizi wa madawa na ubadhirifu wa madawa: Je, nini mkakati endelevu wa Serikali kuhakikisha kwamba wizi wa dawa unadhibitiwa na dawa zinapatikana muda wote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, Mheshimiwa Mnzava ameuliza kuhusu majengo mengine. Kwa bajeti ya mwaka huu 2021 Serikali imetenga shilingi bilioni 4.5 kwa ajili ya majengo mengine ambayo ameyataja.

Vilevile imetenga shilingi bilioni 1.9 kwa ajili ya magonjwa ya mlipuko. Kwa maana kwa bajeti mwaka huu tunaokwenda kuanza, kuna shilingi bilioni 6.4 ambazo zinaenda kuelekezwa kwenye hospitali husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, ameuliza ni kwa namna gani tunaenda kudhibiti wizi wa madawa kwenye hospitali zetu. Kwanza, niseme tu kwamba tumepita na tumegundua kwamba watumishi wengi wa Wizara ya Afya wanafanya kazi nzuri sana lakini kuna wachache ambao wanafanya haya mambo ya ubadhirifu. Vile vile tumegundua kwamba wabadhirifu wamekuwa wakienda Mahakamani aidha, wanaishinda Serikali au kesi zinachukua muda mrefu. Kwa hiyo, tunaenda kimkakati sana kuhakikisha kwamba yeyote atakayepatikana hachomoki, ni lazima awajibike.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, baada ya miezi miwili, mtaanza kuona mkakati wa Wizara wa kuhakikisha moja kwa moja hayo mambo yamefutika, kwa sababu watu wako chini kuhakikisha kwamba tukianza kufanya hiyo kazi hakuna atakayechomoka na tunamaliza hilo tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Viwanda. Tunazungumzia uchumi wa kati ikiwemo kuondeleza viwanda vyetu, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, ni nini mpango wa Serikali katika kuongeza viwanda vingi ili hawa vijana wanaohitimu mafunzo haya waweze kupata ajira kwa sababu naona ni vijana saba tu ambao wameajiriwa na Serikali?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, ni nini mpango mkakati wa Serikali kufufua viwanda vyote ambavyo vilijengwa enzi za Mwalimu ili hawa vijana wetu akribani 228 waliohitimu mafunzo haya ambao hawajapata ajira waweze kuajiriwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Tanzania tupo katika mkakati wa kuwa na uchumi unaoendeshwa na viwanda na hasa tukiwa sasa tumefika katika uchumi wa kati. Mpango wa Serikali ni kuhakikisha tunaongeza viwanda vingi kwa kuhamasisha sekta binafsi kupitia kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya wadau wa viwanda kuwekeza katika viwanda vingi ambavyo hatimaye vinatumia vijana wetu wanaohitimu katika vyuo vingi ambavyo vinatoa elimu hususan inayolenga katika kuongeza ubora wa bidhaa zetu zinazozalishwa katika viwanda lakini pia lengo ni kuona sasa tunakuwa na viwanda ambavyo vitakuwa vinapata wataalam walio na utaalam mahsusi katika mahitaji wa viwanda hivyo. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kuhamasisha sekta binafsi lakini pia mashirika na watu mbalimbali na wawekezaji kutoka nje ambao wanaweza kuwekeza katika viwanda hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili ni kweli viwanda vingi vilivyokuwa vimejengwa wakati wa enzi za Nyerere lakini pia viwanda vingi ambavyo vilikuwa vimebinafsishwa havifanyi kazi. Serikali ina mkakati maalum kwanza kupitia viwanda vyote ambavyo havifanyi kazi, lakini hasa vile ambavyo vilikuwa vimebinafsishwa kwa watu ambao hawaviendelezi ili tuweze kuvifufua. Lengo ni kuona sekta ya viwanda inaendelea lakini wa kutumia miundombinu ya viwanda iliyokuwepo hapo kabla ili viweze sasa kuchukua wataalam wengi ambao wanasoma katika vyuo vyetu vingi ili waweze kuajiriwa katika viwanda hivyo.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa changamoto ya Barabara ya Kairuki ni sawa kabisa na changamoto iliyopo katika barabara ya kutoka Ndala kwenda Mwawaza kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. Je, ni lini Serikali itatoa fedha kukamilisha barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameainisha Barabara ya Ndala – Mwawaza kuelekea Hospitali ya Shinyanga. Ameuliza ni lini Serikali itaikamilisha. Niseme tu kwamba, tutaikamilisha kwa kadri ya upatikanaji wa fedha na tathmini ambazo zinaendelea kufanyika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge awe na subira, hiyo barabara itajengwa kwa kadri tutakavyopata fedha. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa ajili ya majibu ya Naibu Waziri. Maswali mawili ya nyongeza; nini commitment ya Serikali kuhusu tabia ya kuzichelewesha fedha na baada ya muda mfupi kuzirejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili…

SPIKA: Rudia la kwanza.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Nini commitment ya Serikali kuzichelewesha fedha kuzipeleka Halmashauri na baada ya muda mfupi kuzirejesha?

SPIKA: Swali lako halisomeki, la pili na la mwisho.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Je, halmashauri itakuwa…

SPIKA: Aah! Umechelewesha unarejeshaje tena ulichokichelewesha.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: mfumo unazichukua zile fedha…

SPIKA: Naam.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Kwamba inachelewesha kutuma fedha mpaka mwezi wa tano au wa nne lakini baada ya muda mfupi tu mfumo unazirejesha kwenda Hazina kabla zile fedha hazijatumika.

Nini commitment ya Serikali… (Makofi)

SPIKA: Rudia mara ya mwisho.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Swali la mwisho je Halmashauri…

SPIKA: Hilohilo hujaeleweka

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Sijaeleweka, nasema hivi…

SPIKA: Unajua anatoka Shinyanga ni Msukuma huyu sasa inakuwa tabu kidogo.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Nini commitment ya Serikali kuhusu suala la kuchelewesha fedha kuzituma katika halmashauri husika na baada ya muda mfupi kuzirejesha kupitia huo mfumo?

SPIKA: Yaani anachosema hela inacheleweshwa kupelekwa kwenye halmashauri hadi kwenye mwezi wa nne/ tano si bajeti inaisha mwezi wa sita halafu wakishazituma kwenye halmashauri mwezi ule wa nne/tano baada ya wiki mbili/tatu wanazichukua tena fedha zilezile ndicho anachojaribu kukieleza. (Makofi)

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa elaboration.

SPIKA: La mwisho.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, la mwisho; je, halmashauri itakuwa inatenda kosa ikizikatalia zile fedha zisirejeshwe kwenye mfumo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Bajeti Na. 11 ya mwaka 2015 inaeleza vizuri utaratibu wa fedha zinazopelekwa kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo zimepangiwa majukumu mahususi lakini hazitatumika mpaka tarehe 30 Juni ya mwaka husika wa fedha.

Utaratibu uliolekezwa na sheria ni kwamba Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wakishaona fedha zimeingia kwa kuchelewa na kwa mazingira halisi hawawezi kuzitekelezea majukumu yake by tarehe 30 Juni ya mwaka husika wanatakiwa kuandika barua kwa Katibu Mkuu Hazina kupitia Katibu Mkuu TAMISEMI kuomba maombi maalum na kutoa sababu za msingi kwamba fedha zile hazitaweza kutumika kwa tarehe husika na hivyo wapewe kibali maalum cha kutumia fedha zile ndani ya robo ya kwanza ya mwaka wa fedha unaofuata kwa maana ya Julai, Agosti na Septemba ya mwaka wa fedha unaofuata.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo, Wakurugenzi wengi wamekuwa hawaitekelezi ipasavyo sheria hiyo na nichukue nafasi hii kutoa wito na maelekezo kwa Wakurugenzi wa halmashauri kwanza kuhakikisha wanaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mara wanapopokea fedha lakini pili kutekeleza sheria hiyo kwa kuomba kibali maalum cha matumizi ya fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, pili; mifumo ambayo kimsingi inatumika katika kupeleka hizi fedha na kutumia katika mazingira hayo zina changamoto zake lakini Serikali inaendelea kuboresha kuhakikisha karibu na mwisho wa mwaka mifumo hii inafanya kazi na kuwezesha miradi ya maendeleo kutekelezwa.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Kwa kuwa katika majibu yake ya msingi amesema kwamba mradi wa muda mrefu wa Shelui – Tinde utaweza kukidhi mahitaji ya wananchi wa Shinyanga: Je, ni lini sasa Mradi wa Shelui –Tinde utaanza kwa kuwa mkataba umeshasainiwa toka tarehe 25 mwezi wa Pili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa tunajua Sera ya Maji ni kuhakikisha kwamba inasambaza maji katika vijiji vyote ambavyo vinapitiwa na bomba kuu la Ziwa Victoria.

Je, ni lini Serikali itaanza kusambaza maji katika Kata za Lyabukande, Lyamidati, Nindo, Imesela na Didia?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mradi huu kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi tunatarajia kutoa maji Ziwa Victoria na Shelui – Tinde pia itakuwa ni moja ya wanufaika mwaka ujao wa fedha, kadiri fedha tunavyozipata.

Mheshimiwa Mwenyrkiti, napenda sana kumshukuru Mheshimiwa Rais, tumesikia jana wakati Bajeti ya Serikali Mheshimiwa Waziri akihitimisha pale, Mheshimiwa Rais ametuongezea fedha ambazo zitatusaidia kuongeza maeneo mengi katika nchi hii kuhakikisha maji ya uhakika yanakwenda kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile suala la usambazaji maji katika miradi yetu hii ni lazima ifanyike. Lengo ni kuona kwamba, wananchi wanapelekewa maji karibu na makazi yao na kupunguziwa umbali mrefu wa kutembea. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa matumizi ya zebaki, hasa Kanda ya Ziwa, sehemu ambazo wanachimba madini imekuwa ikisababisha ongezeko la wagonjwa wa Kansa ya Shingo ya Uzazi: Je, Serikali imeshafanya utafiti kuthibitisha kwamba zebaki ndiyo chanzo cha ongezeko la magonjwa ya kansa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba hata ukienda Ocean Road imeonekana kwamba wagonjwa wengi wenye matatizo ya kansa wanatokea Kanda ya Ziwa. Hayati Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli aliwahi kuagiza ufanyike utafiti ambao bado majibu yake hayajaja ili kuthibitisha nini hasa chanzo cha tatizo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachofanyika kwa sasa ni kwamba kwanza kuna sababu nyingi ambazo zinasababisha kansa ya kizazi. Kwa hiyo, hatuwezi kusema specifically ni hilo. Kikubwa, tunashirikina na Wizara ya Madini kupitia taasisi yake kuhakikisha sasa wanapochenjua madini, wale wachimbaji wadogo na wakubwa kunakuwepo na control ya kutosha kuhakikisha kwamba haiendi kwenye mazingira na vilevile haiendi kufika maeneo ambayo binadamu wanatumia maji na vitu vingine. Hilo ndiyo tunaendelea nalo kwa sasa.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, katika majibu yake Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba, vituo vya afya vinavyojengwa ni vile vya kimkakati kwa kuangalia na idadi ya watu katika eneo husika. Swali langu; Je, ni lini Serikali itatoa kibali kwa Kituo cha Afya Solwa ambacho kina population kubwa na wananchi wamejitolea kujenga wao wenyewe kile kituo cha afya? Ni lini Serikali itatoa vibali ili kile kituo cha afya cha mkakati kiweze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa vituo vya afya unajumuisha tathmini za kitaalamu za vigezo ambavyo vinakidhi kujenga kituo cha afya. Na mara wataalamu katika halmashauri husika wakishafanya tathmini na kujiridhisha wananchi wanahamasishwa kuendelea kufanya uchangiaji na ujenzi kwa kutumia nguvu zao wakati Serikali pia inatafuta fedha kwa ajili ya kuwaunga mkono.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, Kituo cha Afya hiki cha Solwa kama kimeanza ujenzi, bila shaka wataalamu wamefanya tathmini na hakihitaji kibali cha Serikali maana wataalamu wale tayari wameshafanya tathmini na ujenzi umeanza hakuna kibali maalum ambacho kinatolewa, bali ni kuendelea na ujenzi kukamilisha na kusajili kituo ili wananchi waanze kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kuwaelimisha Ndugu zangu wananchi wa Solwa kwamba, hatuhitaji kibali, lakini tukamilishe ujenzi na kusajili kwa ajili ya kutoa huduma za afya. Ahsante.
SPIKA: Ahsante sana. Nilivyosikia neno kibali hapa nikawa natafakari, Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava ni kibali cha kufanya nini?

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, kituo cha afya kilikuwa dispensary, wananchi wakaongeza kuwa kituo cha afya baada ya lile tamko la kika kata kuwa na kituo cha afya. Kwa hiyo, wananchi wamekwishajenga, wodi zimekamilika, OPD imekamilika, kilichobaki ni TAMISEMI kutoa go ahead ili kile kituo kiweze kufanya kazi.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri nadhani hapo umeelewa hoja yake vizuri. Karibu utoe ufafanuzi.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kimsingi alichokuwa anamaanisha Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava ni kukipandisha hadhi kwa maana ya kukisajili sasa kuwa kituo cha afya na sio kibali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaratibu uko wazi, halmashauri wanaandika barua kwenda Wizara ya Afya kupitia Katibu Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, na tunaipandisha hadhi na kuipa namba ya usajili wa kituo cha afya. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge tutashirikiana kupata documents hizo ili tuweze kukisajili kituo hicho kianze kutoa huduma kwa wananchi kwa ngazi ya kituo cha afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Serikali ina mpango wa kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Ndala kwenda Mwawaza kuliko na Hospitali ya Rufaa. Je, ni lini itaanza kutekeleza mpango huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge Viti Maalum Mkoa wa Shinyanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii itaanza kujengwa pale tu ambapo fedha itapatikana kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hiyo barabara muhimu. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, namshukuru Naibu Waziri wa Afya kwa majibu yake.

Kwa kuwa, umesema kwamba Wizara imekwishafanya ufuatiliaji wa hivyo vifo na sababu zake. Moja ya sababu ni kutokana na matatizo ya dawa za ganzi (nusu kaputi).

Je, kuna watumishi wa kutosha wa kutoa dawa za nusu kaputi katika vituo vyetu vya afya?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa mwaka 2021 ni asilimia 4.1 ya akina mama walipoteza maisha baada tu ya kujifungua kwa oparesheni. Je, kuna utafiti wowote ambao Wizara imeufanya ili kubaini sasa ni dawa gani ambazo zinasababisha akina mama wanapoteza maisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja, anauliza kama tuna uhakika wa kuwa na wataalam wa kutoa dawa ya nusu kaputi kwenye nchi. Juzi mlimsikia Mheshimiwa Waziri wa Afya akieleza kuhusu mkakati wa Rais wetu Samia Suluhu Hassan, ametoa Shilingi Bilioni Nane kwa ajili ya kusomesha wataalam 524 kwa mwaka huu. Mojawapo wa eneo lililoangaliwa ni eneo hilo ambalo kwa kweli kuanzia kwenye hospitali zetu za Wilaya kushuka chini kumekuwepo na watalaam wachache lakini kwa wanaomaliza chuo mwaka huu tutaenda kupunguza hilo tatizo kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili baada ya uchunguzi wetu kwamba imegundulika nini na tunatakiwa kufanya nini kwenye eneo hilo la kupunguza vifo vya akina mama. Moja, ndiyo maana unaona kuna eneo hili la kusomesha, imefanyika kazi kubwa sana, lakini baada ya Serikali yetu kutoa zile fedha za tozo, vituo vya afya 238 vimejengwa kwa mwaka huu tu peke yake. Pia mwaka huu ambulance 663 zinaenda kununuliwa, nazo mnajua zitakavyokwenda kuweza kupunguza kwenye eneo hilo suala la vifo vya akina mama na watoto.

Mheshimiwa Spika, labda nimalize kwa kumjibu namna hiyo.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri. Niliomba kujua dawa ambazo zinasababisha akinamama kufa kutokana na ganzi; naomba sasa Serikali kupitia Wizara ya Afya ifanye utafiti ili tuweze kubaini ni dawa zipi ambazo zinasababisha wanawake wajawazito baada ya kujifungua wafariki? Kwa sababu hapa ametoa sababu nyingine, siyo zile dawa ambazo ilikuwa ni swali langu la msingi. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, labda nimsaidie Mheshimiwa Mbunge kwamba leo mimi niliyesimama hapa huwa nikitumia flagyl nachubuka, lakini mimi kutumia flagyl na kuchubuka, haimaanishi flagyl inachubua watu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anatakiwa kujua kwamba vifo vya akina mama vimepungua kwa zaidi ya nusu kutokana na upasuaji unaofanyika na kutumia ganzi hizi hizi. Maana yake ni nini? Ganzi ambazo tunazozitumia leo hapa Bungeni, tuna Wabunge wengi wamefanyiwa operesheni na wametumia dawa hizi hizi na wako salama. Maana yake ni nini? Tumesema kuna sababu za vinasaba na kuna sababu nyingi ambazo zipo; sasa hizo haziwezi kufanya tukaleta taharuki kwenye nchi.

Mheshimiwa Spika, sisi madaktari huwa ni watu ambao tuna miiko na tunaapa na tuna maadili ya taaluma. Sasa ni muhimu sana unapouliza swali uhakikishe kwamba huvuki ile mipaka ya kitaaluma na miiko kwa sababu kimsingi labda kama angetaka nimweleze ninaposema DNA maana yake nini; ninaposema ganzi, maana yake ni nini? Kwa sababu kuna ganzi ukipigwa hapa kwenye mgongo inasababisha mtu kutokupumua. Kuna procedure za kufanya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nakuomba tuonane kama wanataaluma ili tuweze kusaidiana nawe uelewe jambo linafanyikaje?
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Napenda kujua ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara inayounganisha Wilaya ya Shinyanga Mjini na Shinganya Vijijini kutoka Old Shinyanga kwenda Solo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika,
ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Dkt. Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kwamba kila kitu kipo katika mipango na Serikali tumeainisha maeneo yote yenye vipaumbele. Kwa hiyo, kadri tutakavyoyafikia, maana yake yote yataainishwa. Umuhimu wa hii barabara unafahamika na ndiyo maana mara zote tumekuwa tukifanyia matengenezo. Kwa hiyo, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii na yenyewe itafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli majibu ya Naibu Waziri yananifikirisha sana. Mfadhili ameshapatikana, fedha zimeshatolewa, mkataba umesainiwa mwaka 2017 na wameomba price adjustment. (Makofi)

Je, ni lini Serikali itaongeza hizo fedha ili kazi ianze?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Naibu Waziri amesema kwamba ujenzi utaanza endapo mkandarasi atawasilisha hati ya dhamana ya malipo; ni nini kauli ya Serikali endapo mkandarasi hatawasilisha kwa wakati kama alivyosema kwenye jibu lake la msingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, price adjustment haizuii uwanja kuanza, lakini ni utaratibu kwa kuwa mkataba ulikuwa wa zamani lazima tuwajulishe hawa wafadhili kwamba kutakuwa na ongezeko la bei na endapo pia hawatataka kuongeza Serikali itaendelea kujenga huu uwanja kwa ile nyongeza ambayo itakuwepo kwani tayari wameshatoa milioni 12 United States dollars kwa ajili ya kuanza ujenzi wa viwanja hivyo.

Mheshimiwa Naibu spika, na hati ya dhamana ni kwamba tayari mkandarasi yuko tayari kuanza kujenga na sasa hivi anachofanya tu ni kuandaa hizo hati ili aweze kuziwasilisha baada ya hiyo fedha kutolewa na wafadhili, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga haina kabisa mtandao wa barabara ya lami; je, nini kauli ya Serikali kuhusu kuipatia halmashauri hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ndio maana moja ya mkakati wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI katika bajeti zilizopita ilikuwa ni kutoa shilingi milioni 500 katika kila jimbo ili waanze sasa kujenga mtandao wa lami.

Kwa hiyo, kwa sababu hiyo ahadi inaendelea kutekelezeka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi tutafanya hivyo, lakini mapendekezo makubwa mnayatoa ninyi wenyewe, lakini wazo la Serikali ni kuweka mitandao ya lami katika maeneo yote, ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha katika Wilaya ya Kishapu, vituo vya afya vya Mwahalanga, Dulisi na Kishapu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya awali kwamba mkakati wa Serikali ni kuendelea kuajiri, vituo hivi vya afya ambavyo vina upungufu wa watumishi vitapelekewa watumishi kwenye ajira hii pia kwenye ajira zinazofuata. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa vikundi vingi ambavyo vinapata mkopo wengi wanatoka maeneo ya mijini. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba elimu inatolewa ili wanawake na vijana wa vijijini pembezoni waweze kupata mkopo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika halmashauri zetu zote zikiwemo za vijijini kuna fungu ambalo linatengwa kupitia maafisa maendeleo ya jamii kwa ajili ya kuhamasisha, kuelimisha, wanawake vijana na watu wenye ulemavu kunufaika na fursa za mikopo hiyo. Kwa hiyo suala hilo tunalifanya na jambo kubwa ambalo tunaendelea kulifanya ni kuongeza nguvu ili wananchi wapate nguvu ya kutosha waweze kunufaika na mikopo hiyo.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa kuwa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi imejitahidi kujenga shule za sekondari katika kila kata na kuna watoto wengi hasa wasichana wanatoka wanatembea kilometa zaidi ya tano; je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba shule zinakuwa na mabweni angalau kunusuru watoto wa kike na hawa fataki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba tunajenga shule na mabweni katika maeneo ya pembezoni hususani maeneo yale ya wafugaji zaidi kuhakikisha kwamba watoto wote wanapata ile huduma ya shule bila kwenda umbali mrefu. Kwa hiyo, hilo lipo katika mpango wa Serikali, ahsante.

NAIBU SPIKA: Haya katika mipango yako uweke vilevile na Kisutu Secondary School.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, sawasawa.

NAIBU SPIKA: Imeingia kwenye Hansard hiyo.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, imeingia hiyo.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali imekuwa ikitoa fedha za maendeleo kwenye halmashauri wakati mwingine imekuwa ikitoa fedha mwezi ambao unakaribia mwisho wa mwaka wa fedha kuisha.

Je, Serikali imetatua vipi changamoto hii ya kuchelewesha fedha kwenye halmashauri na baadaye kuzirudisha hazina?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ambazo zinapelekwa kwenye halmashauri zetu karibu na mwisho wa mwaka wa fedha mara nyingi zimekuwa zikirejeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti Na. 11 ya Mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo mahususi yametolewa, kuhakikisha kwamba halmashauri ambazo zinapokea fedha karibu na mwisho wa mwaka wa fedha, ziandike barua kupitia ofisi ya Rais TAMISEMI, kwenda Wizara ya Fedha na Mipango, siku 15 kabla ya tarehe 30 ya mwaka husika, ili zile fedha zisirejeshwe ziendelee na miradi, kwa maana ya quarter ya kwanza ya mwaka wa fedha unaofuata.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Kituo cha Polisi cha Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kilichopo Selamagasi kimejengwa toka enzi ya mkoloni na kimechakaa sana. Je, ni nini mpango wa Serikali kukarabati kituo kile?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, Shinyanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika majibu ya baadhi ya maswali ya Wabunge, tunatambua uwepo wa uchakavu mkubwa kwa baadhi ya Vituo vya Polisi kikiwemo hiki alichokitaja.

Mheshimiwa Spika, kama tulivyosema alivyosoma hotuba ya bajeti ya Wizara hii mpango wa Serikali kuanza ukarabati wa Vituo vya Polisi na makazi katika mwaka ujao na fedha zimepitishwa, tutaangalia kiwango cha uchakavu ili kuweza kuweka kipaumbele vikiwemo hivi vya Wilaya ya Shinyanga.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa barabara ya kutoka Kolandoto kwenda Kishapu ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Kishapu: Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele sana katika kuhakikisha barabara zetu zinapitika wakati wote ikiwemo barabara hii ya Kolandoto kwenda Kishapu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutaliangalia suala hili na kuona ni namna gani barabara hii nayo itaweza kuwekewa fedha na kuweza kutengenezwa.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ni halmashauri kongwe na jengo la utawala halijakamilika. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa jengo la utawala Halmashauri ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilipeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la utawala katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Tunafahamu jengo lile halijakamilika, lakini ujenzi huu unakwenda kwa awamu. Awamu ya kwanza fedha zimepelekwa na kazi ya ujenzi imeanza. Nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha ili ipeleke awamu ya pili kwa ajili ya ukamilishaji wa jengo hilo, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu lakini vitendo vya ubakaji na ulawiti wa watoto wadogo ni vitendo ambavyo vimekithiri katika nchi yetu na moja ya sheria ni kufungwa kifungo cha miaka 30 jela. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kwa sababu ubakaji ni uuaji, kuleta mabadiliko ya sheria ili wabakaji na walawiti wa watoto waweze kuhukumiwa kifungo cha kifo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli anayozungumza Mheshimiwa Mbunge kwamba imekuwepo sheria ya miaka
30 lakini inaonekanika kama ni sheria legevu kidogo naye Mheshimiwa Mbunge anatoa mawazo, anatoa mapendekezo kwa nini isiwepo adhabu hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba tubebe mawazo yake hayo twende tukayafanyie tathmini tuweze kuangalia namna gani sheria hiyo inaweza kubadilishwa.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa Barabara ya kutoka Old Shinyanga kwenda Iselamagazi mpaka Solwa ni barabara ambayo inaunganisha Manispaa na Shinyanga DC.

Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii tumeshaanza kuijenga kwa awamu na tunahakikisha kwamba tayari tumeshafanya usanifu na tutaijenga kwa kiwango cha lami ili kuunganisha Makao Makuu ya Mkoa wa Shinyanga na Halmashauri ya Shinyanga Vijijini. Kwa hiyo mpango upo kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, na pia namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imekwisha kutenga fedha kwa mwaka wa fedha 2022/2023, je, ni lini Serikali itatoa hizo fedha ili ujenzi wa barabara uendelee?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa mkandarasi amekwisha kupatikana, na Naibu Waziri amesema kwamba Septemba ile kazi itakabidhiwa. Je, kwa kuwa mkandarasi amepatikana, ni lini ataanza hiyo kazi ili Septemba aikabidhi?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mkandarasi akishakabidhiwa anachofanya ni maandalizi ya ujenzi, na kwa hiyo kwa kuwa tumeshamkabidhi, na tumekubaliana lini atamaliza kazi, mkandarasi yuko site kwa maana ya kufanya maandalizi, na mwezi Septemba tunategemea atakuwa amekamilisha hiyo kazi, na kadri Serikali itakavyoendelea kupata fedha, barabara hii tuna uhakika itakamilishwa yote, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Makamu wa Rais alivyokuwa Shinyanga aliahidi barabara ya kutoka Ndala kwenda Mwawaza ambako kuna Hospitali ya Rufaa, ingetengenezwa kwa kiwango cha lami.

Ningependa kujua ni lini itaanza kutengezenzwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge barabara hii ni ahadi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, vilevile inaunganisha huduma muhimu kwenye jamii kama vile Hospitali hii ambayo iko hapo, hivyo basi Serikali itaipa kipaumbele na kutekeleza utekelezaji wa barabara hii kama ilivyokuwa maelekezo ya Makamu wa Rais lakini vilevile ni uhitaji mkubwa wa wananchi wa Shinyanga.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa Hospitali ya Manispaa ya Kahama inatibu kama hospitali ya mkoa; ni nini kauli ya Serikali kuhusu kuongeza idadi ya watumishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwenye ajira hizi ambazo Serikali imetangaza na ambazo mchakato unaendelea tutahakikisha hospitali ya Manispaa ya Kahama nayo inapata watumishi wa kutosha kuweza kusaidia wananchi wa pale Kahama.
MHE. DKT. CHRISTINE C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Serikali iliahidi kuvipatia umeme vijiji vilivyopo katika Kata ya Mwamalili, Kolandoto, Chibe, Mwawaza na Old Shinyanga; je, ni lini Serikali itavipatia umeme vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, Shinyanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote ambavyo havikuwa na umeme na havina umeme hadi sasa viko katika Mradi Mkubwa wa Umeme wa REA, awamu ya tatu, mzunguko wa pili. Kufikia Desemba, 2023 tuna uhakika vijiji hivyo vitakuwa vimepata umeme kupitia mikataba ambayo tuko nayo na inayoendelea kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mradi huo ndio tunamshukuru Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza kilomita mbili katika ile kilomita moja tuliyokuwa nayo awali. Kwa hiyo wigo wa mradi utakuwa ni mpana zaidi kuweza kuwafikia wananchi wengi katika vitongoji kwa ajili ya kupata maendeleo kwenye maeneo yao.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Kwa kutambua kwamba Solwa inahudumia watu karibia 31,000 na imebeba jina la Jimbo la Solwa; napenda kujua, Mganga Mkuu atatumia siku ngapi kumaliza ukaguzi huo? Swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na sehemu nyingine wamekuwa wakijitolea kuongeza majengo ya zahanati ili yaweze kuwa vituo vya afya ili kukidhi huduma, sasa napenda kujua, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba zahanati zote ambazo zinakidhi na zimeshaongeza majengo, zitabadilishwa kuwa vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ni siku ngapi zitachukuliwa kwa ajili ya ukaguzi huu wa Zahanati ya Solwa ambayo inahudumia watu 31,000 katika Jimbo la Solwa, nitoe agizo kwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja, taarifa hii iwe imefika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kuona zahanati hii inaanza mchakato wa kupandishwa hadhi na kuwa kituo cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili la Mheshimiwa Dkt. Mnzava kwamba wamejenga zahanati nyingi katika maeneo ya kimkakati, ni lengo la Serikali kuhakikisha kwamba zahanati hizi ambazo zimejengwa kwa nguvu ya wananchi kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu ya Tanzania, siyo Shinyanga peke yake kwamba zinapatiwa fedha na kuweza kuwa upgraded yale kwa yale maeneo ya kimkakati, na Serikali itafanya hivyo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu ya Serikali. Kwa kuwa mradi huu ulianza 2012 na 2013 mkandarasi akaondoka na gharama yake ni takribani bilioni 1.4 je, Serikali inatoa ahadi gani kwa wakazi wa Ishololo Usule? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa mradi huu ni muhimu sana kwa wananchi wa Ishololo Kata ya Usule je, Waziri uko tayari kutembelea mradi huu ukaone ni jinsi gani wananchi wa Ishololo – Usule wanauhitaji wa mradi huu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge, kwamba Waziri yuko tayari kufika katika eneo la Ishololo – Usule ili kujionea hali halisi ya huo Mradi. Commitment ya Serikali ni kama katika jibu la msingi lilivyoandikwa kwamba katika mwaka wa fedha huu unaokuja 2023/2024 tutafanya tathimini na utekelezaji wa huu mradi utaanza 2024/2025.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Kata za Masanga na Ngofia katika Jimbo la Kishapu hazina mawasiliano kabisa ya simu. Je, ni lini Serikali itapeleka minara katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kati ya majimbo ambayo yamepata minara mingi sana, minara zaidi ya tisa ni katika Jimbo la Kishapu na utekelezaji wake uko katika hatua mbalimbali na umeshaanza. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kushirikiana na watoa huduma ili miradi hii ikamilike kwa wakati, ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kata ya Isalamagazi ambayo ndiyo Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kuna kituo cha polisi ambacho kimejengwa enzi za mkoloni.

Je, ni lini Serilkali itajenga kituo hicho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali inatambua uchakavu wa baadhi ya vituo vya polisi na hata baadhi ya makazi ya Askari Polisi. Ndiyo maana Serikali tumo kwenye mbio ya kuhakikisha tunatafuta fedha ili tujenge vituo vya kisasa zaidi na viweze kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba Serikali tutakapopata fedha tutahakikisha kituo chake tunakipa kipaumbele ili wananchi waweze kupata huduma za ulinzi na usalama. Ninakushukuru.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Mahakama ya Mwanzo ya Usanda katika Wilaya ya Shinyanga imechakaa. Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Mahakama hiyo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wetu wa Shinyanga tunakwenda kujenga katika mwaka huu wa fedha katika Tarafa ya Majengo, Kata ya Malunga naomba ni-check na Mheshimiwa Dkt. Mnzava ili tuone kwamba Mahakama hiyo ambayo imechakaa tuweze kuingiza kwenye mpango unaofuata wa Mahakama ya ujenzi. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi hii. Kwa kuwa Halmashauri zote za Mkoa wa Shinyanga hasa vijijini zina upungufu mkubwa wa wafanyakazi. Je, ni nini kauli ya Serikali kutatua tatizo hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Dkt. Mnzava kwamba, Serikali itaendelea kutatua upungufu wa watumishi wa umma ikiwemo Walimu katika Mkoa wa Shinyanga na mikoa mingine hapa nchini kadri ya bajeti yake itakavyoruhusu na ndio maana katika bajeti ya 2022/2023 Serikali ilitenga ajira 21,000 kwa ajili ya Walimu na kada ya afya, kwa ajili ya kupunguza upungufu uliopo kote nchini ikiwemo kule Shinyanga.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kuwa Mahakama za Usanda na Samuye katika Halmashauri ya Shinyanga zimejengwa toka enzi ya mkoloni. Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Mahakama hizo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru nijibu swali la Mheshimiwa Mnzava Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Shinyanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wetu wa Mahakama mwaka huu tunakwenda kujenga Mahakama zaidi ya 38 za Wilaya, Mahakama 60 za mwanzo lakini pia fedha hizi ambazo tumetenga tunakarabati pia Mahakama.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Mnzava nipokee Mahakama ambazo umezitaja tutaweka kwenye mpango wetu wa Mahakama ili tuzikarabati.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa Kata ya Didia ni Kata ya kimkakati na ina idadi kubwa sana ya watu ukizingatia kwamba ni maarufu kwa zao la mpunga.

Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali hii ya Awamu ya Sita kuhakikisha inajenga vituo vya afya kwenye maeneo yote ya kimkakati nchini, ikiwemo Kata hii aliyoitaja Dkt. Christina Mnzava, tutafanya tathmini na kuona mahitaji yanayohitajika pale na kisha kuiweka kwenye mipango yetu ya kutafuta fedha. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Kata ya Mwasubi iliyopo katika Tarafa ya Mondo, Wilaya ya Kishapu ni kata mpya na haina madarasa ya kutosha katika shule ya sekondari. Je, ni lini Serikali itajenga ili kuongeza madarasa katika shule hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge tutaongeza madarasa kwa kuwa moja ya mpango wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kuhakikisha shule zote tunazifikia kwa kuongeza madarasa na kuzikarabati. Ahsante sana.
MHE. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, Hospitali ya Kahama inahudumia watu kutoka pembezoni kwa maana ya Mikoa ya Tabora pamoja na Geita. Je, ni lini Serikali itaboresha kituo cha Watoto njiti pale Hospitali ya Kahama?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, kwanza nijibu swali la Mheshimiwa hapa, ukisikia Serikali inasema inajenga vituo vya afya kwa kila Tarafa na kazi ile imeendelea kufanyika kupitia TAMISEMI ni kwenda kupunguza wagonjwa ambao sasa wanaenda kurundikana kwenye hospitali moja kama ilivyo Kahama.

Mheshimiwa Spika, mimi nafikiri Mbunge ni muhimu tukatembelea hospitali hiyo inawezekana tukikaa mle ndani tutaona tu maeneo ambayo tunaweza tukaweka sehemu ya Watoto njiti, ibaki kazi ya kuleta vifaa na kuvipachika na Watoto waweze kupata huduma.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa stendi ya mabasi ya Shinyanga Manispaa imechakaa na ni ya zamani haijajengwa kisasa, je, ni lini Serikali itajenga Stendi Kuu ya Mabasi, Manispaa ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, stendi hizi zote kama nilivyotangulia kujibu kwenye jibu la awali la halmashauri husika, Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, wafanye tathmini na kuona gharama ambazo zinahitajika kukamilisha au kujenga stendi ile, lakini waone uwezo wao wa mapato ya ndani kutenga kwenye bajeti. Kama inahitaji gharama kubwa, walete andiko hilo Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ili tuweze kufanya tathmini na kutafuta vyanzo vya fedha. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; kwa kuwa watu wengi wenye ulemavu wa ngozi hawako kwenye vituo, wengine wako vijijini; je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba hata wale ambao hawko kwenye vituo vya Watoto walio na albinism.

Je, nini mkakati wa Serikali kuwafikia kule waliko kuwapa mafuta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba siyo wote wenye ulemavu wa ngozi (ualbino) wapo kwenye vituo vya huduma, kwa maana ya watoto, lakini hapa tunaongelea watoto na watu wazima kupata huduma hii. Sasa utaratibu ambao tutauweka, kwanza tukisogeza huduma hizi za mafuta karibu na zahanati na vituo maana yake wale watu wenye ualbino watajua kwamba mafuta yakiisha watakwenda kwenye zahanati ya karibu zaidi au kwenye kituo cha afya au hospitali ya karibu zaidi. Kwa hiyo, mpango wa Serikali ni kusogeza zaidi upatikanaji wa huduma hii kwenye vituo katika jamii zetu, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Kata ya Mwasubi iliyopo katika Tarafa ya Mondo, Wilaya ya Kishapu ni kata mpya na haina madarasa ya kutosha katika shule ya sekondari. Je, ni lini Serikali itajenga ili kuongeza madarasa katika shule hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge tutaongeza madarasa kwa kuwa moja ya mpango wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kuhakikisha shule zote tunazifikia kwa kuongeza madarasa na kuzikarabati. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa changamoto ya vifaa katika Jeshi la Zimamoto ni mtihani hasa katika Manispaa ya Shinyanga.

Mheshimiwa Spika, unaunguliwa mita 100 zimamoto inakuja inashindwa kuzima moto, je, ni lini Serikali itaboresha miundombinu ya zimamoto katika Manispaa ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ipo mikakati mingi ambayo tunaitumia katika kuboresha, moja; ni ajira kwa kuongeza nguvu kazi lakini pili manunuzi ya vifaa mmetupitishia bajeti hivi juzi zaidi ya bilioni 11 zinakwenda kununua vifaa ambavyo vitapeleka kwenye maeneo yenye changamoto kubwa ikiwemo Mkoa wa Shinyanga. Nashukuru.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi; kwa kuwa Serikali imeamasisha wananchi kujenga zahanati katika kila kata na vijiji na maboma mengi hayajakamilika, je, nini kauli ya Serikali kukamilisha maboma hayo katika Halmashauri ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali ilihamasisha wananchi kwa nia njema ya kuhakikisha kwamba wananchi wanapata zahanati na vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati na mpango wa Serikali ni kukamilisha zahanati na maboma ya vituo hivyo katika maeneo ya kimkakati kwa maana ya kata za kimakakati na tarafa za kimkakati, siyo kila kata au siyo kila kijiji na kazi hiyo imefanyika sana kwa mfano katika mwaka mmoja maboma ya zahanati 954 yamekamilishwa, mwaka ujao Serikali imetenga bilioni 15 kwa ajili ya kukamilisha maboma 300 ya zahanati, kwa hivyo kazi hii itaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.