Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Dr. Christina Christopher Mnzava (1 total)

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kunipa nafasi kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ongezeko kubwa sana la vituo vya afya na zahanati nchini baada ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa fedha za UVIKO-19. Palipo na mafanikio changamoto hazikosekani. Kumekuwa na uhaba mkubwa wa watumishi wa kada ya afya.

Mheshimiwa Spika, je, ni nini mkakati wa Serikali kukabiliana na changamoto hii?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba Serikali, na kwa maelekezo ya Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ya kutaka kuboresha huduma za afya Serikali imefanya uwekezaji mkubwa kwenye maeneo ya kutolea huduma, zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, hospitali za mikoa na hospitali za kanda, lakini pia hospitali kuu kama vile Benjamini Mkapa na maeneo mengine tumepanua maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, tunatambua uwekezaji huu ni mkubwa. Tumeanza na kuweka miundombinu, tumepeleka vifaa na maeneo mengine bado vifaa vinapelekwa, na mimi nimefanya ziara maeneo mengi, nimekuta vituo vya afya, zahanati hata hospitali bado tunaendelea kupeleka vifaa. Hata hivyo, vifaa hivi lazima viende sambamba na watumishi wa kada hii ya afya ambayo umesema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi wakati wa bajeti ya Wizara ya Afya hapa tumepata taarifa kwamba Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan ameshatoa kibali cha ajira, na kibali hiki kiko kwenye sekta za afya, elimu, kilimo, fedha na utawala. Kwa hiyo, tunatarajia baada ya kibali hiki kuwa kimeshakamilika taratibu zake tutapeleka watumishi wa afya kwenye maeneo haya yote mapya ili huduma ianze kutolewa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na Watanzania wote wanamshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye sekta ya afya. Anataka kuona jamii ya Watanzania ikipata huduma kwenye maeneo yao kwa ukaribu, anataka kuona Watanzania wanatumia gharama ndogo kwa kupata huduma karibu na maeneo yao, na sisi tuendelee kumuunga mkono kama ambavyo tunamuunga mkono na tuamine kwamba mkakati huu wa Serikali wa kupeleka watumishi wa umma utakamilika katika kipindi kifupi sana kijacho. Hii ni kwa sababu tayari fedha ipo (Hapa ilikata) kwa sababu tayari fedha ipo na Waheshimiwa Wabunge mmeridhia. Jukumu letu kuanzia tarehe mwezi wa saba na kutoa fedha na ajira ipatikane na watumishi waanze kazi. Ahsante sana. (Makofi)