Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Christina Christopher Mnzava (14 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kusimama na mimi kwa mara ya kwanza katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema kwa kunijalia nami kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge la Kumi na Mbili. Vilevile namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uhai wa kutuwezesha Wabunge sote kwa pamoja kuja katika Bunge hili na kuwatumikia wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja kwa moja naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia katika suala la afya. Tumeona ni jinsi gani Mheshimiwa Rais ameweza kutupa dira ambayo itatufanya tufikie katika malengo ambayo tumeyakusudia. Kwa mfano, kwa mwaka 2015 tumeona kwamba mpaka kufikia 2020 Zahanati zimekukwa 1,198, Vituo vya Afya 487 na Hospitali 99.

Mheshimiwa Spika, pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kwani alipokuwa kwenye ziara Mkoa wa Shinyanga, Wilaya ya Kahama, aliipandisha hadhi kuwa Manispaa na Hospitali yetu ya Wilaya ya Kahama inatarajiwa kupanda daraja. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo anazidi kujidhatiti katika kuboresha huduma za afya kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, katika kipengele hiki cha sekta ya afya, nakumbuka kulikuwa na mpango wa MMAM. Mpango huu ulikuwa umekusudia kila Kata kuwa na Kituo cha Afya na kila kijiji au mtaa kuwa na Zahanati. Katika Mkoa wa Shinyanga kuna zahanati nyingi ambazo zimeshafika kwenye maboma. Hivyo, nadhani ni wakati muafaka sasa, ili kutimiza azma na matamanio ya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha kwamba huduma za afya zinawafikia Watanzania wengi, yale maboma yaweze kumaliziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala zima la afya, tumeona jinsi ambavyo vifo vya wamama wajawazito vilivyopungua kutoka vifo 11,000 mpaka vifo 3,000. Hili tuna sababu kubwa sana kumpongeza Mheshimiwa Rais na watendaji wote wa Wizara ya Afya na wafanyakazi wote wa sekta mtambuka ambao wanahakikisha kwamba huduma ya afya inaimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo la maji, lakini tumeona dira ambayo Mheshimiwa Rais ameionyesha katika hotuba yake na vilevile kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, nawapongeza sana Wizara ya Maji, hasa Mheshimiwa Aweso kwa kazi kubwa anayoifanya pamoja na watendaji wote wa Wizara hiyo ya Maji kuhakikisha kwamba mwanamke anatuliwa ndoo hasa katika Mkoa wa Shinyanga, Tabora na hata Dodoma kwa kweli sasa hivi shida ya maji siyo kama ile. Tunatarajia kwamba mradi wa Ziwa Victoria utafika na Dodoma na sehemu nyingine. Kwa hiyo, ni suala la kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa juhudi ambazo kwa kweli anazifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, tumeona katika suala zima la uchumi. Ukiangalia katika hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Rais mwaka 2015 ukalinganisha na hotuba ambayo ameitoa mwaka 2020, tunaona kuna ongezeko la pato la Taifa kutoka 7% kwa mwaka. Pia tumeona makusanyo ya mapato yameongezeka toka shilingi trilioni 94.3 kwa mwaka 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 139. Hivyo tuna sababu kabisa ya kuweka mipango yetu vizuri kwa sababu tunakwenda kwenye bajeti. Katika bajeti ni lazima tuzingatie dira ambayo Mheshimiwa Rais ameitoa ili tuweze kutekeleza yale ambayo Chama cha Mapinduzi na sisi Wabunge kwa ujumla tuliyaahidi wakati tunaomba kura.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuzungumzia kuhusu barabara. Barabara ni changamoto sana hasa vijijini. Hata hivyo, kwa mpango madhubuti ambao upo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, naamini kwamba kuja kufikia 2025 barabara nyingi zitakuwa zinapitika na zinafunguka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda kusema kwamba kwa kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais, sisi kama Wabunge tuna sababu ya kumpongeza na kuzidi kumwombea kwa sababu vita ya kiuchumi ni kubwa sana. Mheshimiwa Rais naamini halali akiwaza maendeleo ya Tanzania, anatamani kuacha nchi ya Tanzania katika level fulani na anatama yale anayoyafikiria yanatimia. Hivyo, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba tunamwombea.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, niseme kwamba tunapaswa kuendelea kumwomba Mungu hasa katika janga ambalo lipo lakini tunapaswa kuendelea kujikinga kwa sababu Mungu wetu ni mwaminifu, kama ambavyo aliweza kutushindia kipindi kile tukaweza kuepukana na janga hili, ataendelea kutushindia. Nchi za wenzetu wanatamani kuwa na Rais kama Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Wanasema laiti tungekuwa tunaweza kubadilishana, basi tungeweza kubadilishana mkatupa Rais Dkt. John Pombe Magufuli hata kwa mwaka mmoja. Kwa hiyo, tuna sababu sanasana sana ya kumshukuru Mungu kwa sababu ya kumpata Rais huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, natumia fursa hii kukushukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuweza kuchangia taarifa ambazo zipo mbele yetu. Kwanza niwapongeze sana Wenyeviti wote wa Kamati hizo tatu ambazo tunazijadili leo, lakini niipongeze sana Serikali kwa juhudi kubwa ambayo inafanywa ya kuwekeza kwenye taasisi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tuna jumla ya takribani mashirika na taasisi 237 na kati ya hizo 10 zimewekeza nje ya nchi yetu ya Tanzania. Kwa mwaka 2020/2021, Serikali imekwishawekeza mtaji wa thamani ya shilingi trilioni 67 na point. Kwa kweli ni juhudi kubwa sana na Serikali inafanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na uwekezaji huo ambao ni zaidi ya asilimia 63.8 toka ilipoanza kuwekeza mwaka 2016/2017, ilikuwa kama trilioni 49 na kidogo, lakini mpaka 2020/2021 tumefikia trilioni 67, kwa kweli ni uwekezaji mkubwa ambao Serikali inaufanya.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Kamati ya Uwekezaji Mitaji ya Umma kwa kweli tumeshuhudia kwa macho kuona ni jinsi gani Serikali yetu ya Tanzania chini ya Mama Samia Suluhu Hassan inawekeza.

Mheshimiwa Spika, mbali na kuwekeza bado kuna changamoto. Changamoto kubwa ambazo tumeziona ni pamoja na kutokuwa na Bodi za Wakurugenzi kwa wakati kwa baadhi ya Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma. Kusipokuwepo na hizi Bodi za Wakurugenzi, usimamizi wa fedha ambayo Serikali imewekeza unakuwa na mashaka. Kuna taasisi zaidi ya miaka miwili haina Bodi ya Wakurugenzi.

Kwa mujibu wa Sheria kama Bodi ya Wakurugenzi haipo. Katibu Mkuu wa Wizara husika anawajibika kusimamia ile Taasisi, naye ana muda wake wa kusimamia ile taasisi si zaidi ya miezi kumi na mbili, lakini unakuta Katibu Mkuu bado anasimamia hiyo taasisi zaidi ya miaka miwili, ufanisi unakua mdogo, ufanisi unakuwa na mashaka.

Mheshimiwa Spika, tunakumbuka mwezi Machi, 2022 wakati Mheshimiwa Rais anapokea ripoti ya CAG alitamka akasema yeye masuala mazima ya uteuzi ya hizi bodi yakifika mezani kwake hachukui muda kuyasaini na kazi zikaendelea. Hivyo basi, tuwaombe Wizara na Taasisi ambazo zinasuasua au kuna delay fulani ya kuteua hizi Bodi za Wakurugenzi, basi ziweze kufanya hivyo ili taasisi na fedha hiyo ambayo ni ya Watanzania imewekezwa iweze kuwa na tija. Kuna taasisi zingine ambazo zinachelewa sana kupata vibali vya ajira, unakuta ina watumishi wachache, unakuta kuna watumishi wa muda, lakini unaweza ukakuta tena kuna watumishi ambao wanakaimu zaidi ya miaka sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mtu anapokaimu kwenye position moja zaidi ya miaka sita, mitano hata ile confidence ya kufanya kazi anakuwa hana. Anakuwa hana maamuzi kamili ya kuweza kufikia maamuzi ili taasisi iweze kusonga mbele. Nashauri mamlaka husika waweze kufuatilia kujua kwamba ni taasisi ngapi ambazo zina matatizo au changamoto hizo. Tunamshukuru sana na kumpongeza sana TR, amekuwa akifanya kazi kubwa sana kuhakikisha kwamba anasimamia haya Mashirika ya Umma yanafanya kazi zake kwa ufanisi, lakini kuna mambo mengine ambayo kama Serikali, kama Wizara, kama Taasisi husika ni lazima waweze kufuatilia.

Mheshimiwa Spika, vilevile ningependa kuchangia kujikita kwenye Shirika moja la Umma ambalo kwangu naona kama ni uti wa mgongo, Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (Tanzania Agricultural Development Bank). Benki hii inamalengo yake matatu, naomba niyarejee; la kwanza ni kusaidia utoshelezi wa usalama endelevu wa chakula Tanzania. Lengo la pili ni kuchagiza mapinduzi ya kilimo kutoka kilimo cha kujikimu kwenda kwenye kilimo cha biashara. Lengo la tatu, ni kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi. Ni ukweli usiopingika, kilimo ndio ndio uti wa mgongo kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ambayo tumeipitisha mwaka huu Wizara ya Kilimo imetengewa zaidi ya bilioni 900 na kidogo. Ukiangalia Benki hii inawajibika moja kwa moja kwa wakulima wa Nchi yetu ya Tanzania. Ukiangalia tena mtaji ambao wanao hii Benki ya Maendeleo ya Wakulima Tanzania, bado haukidhi. Kwanza Benki yenyewe iko Stationed Dar-es -Salam, mikoani kule ambako kuna wakulima, mikoa ya pembezoni hakuna tawi lolote. Sasa nashauri kwamba, Serikali kwa sababu ilishaji-commit kuwapa mtaji hii benki na iliahidi kuwapa bilioni 700 na ikasema itakuwa inatoa bilioni 100 kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi tunapoongea Benki hii imekwishapewa bilioni 208 ina jumla ya mtaji bilioni 268, bado ni kidogo sana kwa majukumu ambayo benki hii inayo ya kuhakikisha kwamba kilimo cha umwagiliaji Tanzania kinakua, kuhakikisha kwamba wakulima wa kule Shinyanga, Songwe na Tanzania nzima wananufaika na hii mikopo ya benki hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiiwezesha Benki ya Kilimo, tukawa-link na Wizara ya Kilimo ambapo Wizara ya Kilimo ina fedha ambazo zinakwenda moja kwa moja kwenye kilimo cha umwagiliaji, wana fedha ambazo zinakwenda kukopesha na kuwapa wakulima pembejeo, kuna fedha ya ufuatiliaji na usimamizi, lakini kuna fedha ya kuweza kuwapa miundombinu kama matrekta wakulima wadogo wadogo. Benki hii ikiwa linked pamoja na Wizara ya Kilimo ikasimamia zile fedha ambazo tunategemea wakulima wa Tanzania wakopeshwe waweze kutengeneza kilimo cha umwagiliaji, waweze kukopa matrekta, tunaweza tukawakomboa wakulima wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nishauri kama inawezekana, kama ni sera, sheria au kanuni ziangaliwe tuone ni kwa jinsi gani benki hii itakuwa inafanya kazi kwa karibu sana na Wiizara ya Kilimo ili kuweza kurahisisha kuwakopesha Watanzania pembejeo, matrekta na kuwawezesha kwa namna yeyote ile ili uchumi wetu uweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Benki ambazo zinatoa mikopo kwa wakulima wa Tanzania, lakini Benki yetu ya (TADB) haijawafikia Wakulima wengi. Ukiangalia katika taarifa unaona kabisa kwamba kuna vikwazo ambavyo Serikali inaweza kukaa chini na kuvirekebisha, mfano, wakati benki inahitaji kukopa, labda imepata uhitaji mkubwa wa watu ambao wanahitaji kukopa ili waweze kufanya shughuli za kilimo, lakini kutokana na masharti ambayo yanakuwepo ni lazima Serikali ikope kwa niaba ya ile benki.

Mheshimiwa Spika, kukishindanishwa benki mbili kati ya hii Benki ya Maendeleo ya Kilimo na benki nyingine labda ya binafsi, zote zinakwenda nje ya nchi kwenda kukopa, ukiangalia masharti ya hii Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania na masharti ya benki zingine, unakuta kwenye hii Benki ya kwetu ya Kilimo kuna vikwazo. Ni lazima mchakato ufanyike na unachukua zaidi ya miaka miwili, mitatu, lakini Benki nyingine au Taasisi nyingine ambayo haina milolongo ya vikwazo, haina milolongo ya procedures wao wanakwenda direct kama ni Ufaransa, kama ni Canada wanachukua mkopo, wanakuwa fedha na kuanza kukopesha.

Mheshimiwa Spika, ushindani wa Benki ya Kilimo na ushindani wa benki zingine, kwa kweli benki yetu inaonekana bado haina tija kukidhi soko, kukidhi ushindani ambao benki zingine unazifanya. Ningeshauri tuangalie taratibu zetu kama Serikali, kama nchi kuweza kuinusuru benki yetu hii, kuweza kuiongezea mtaji ili basi hii benki kwanza iwe na matawi mengi Tanzania, iwe na matawi mikoani isikae Dar-es -Salaam peke yake na iwe na matawi sehemu ambazo kweli wanalima. Kwa sababu Dar-es-Salaam wakulima ni wachache, sana sana wengi ni wakulima labda wa Msimbazi pale kulima mbogamboga, lakini wakulima ambao wanaitaji huu mkopo wako mikoani na vijijini.

Mheshimiwa Spika, nashauri kabisa kwamba ni vizuri tukaangalia Serikali ikatoa mtaji ambao iliahidi kila mwaka ingewapa bilioni 100, basi iwape hizo fedha na ikiwezekana iwaongezee zaidi ili Benki yetu sasa iwe na ushindani na iwe na tija na iweze ku-complete na benki zingine na Watanzania wote waweze kunufaika.

Mheshimiwa Spika, sitakuwa na mengi ya kusema kwa leo, isipokuwa nashauri tu kwamba hizo bilioni 700 ambazo Serikali iliahidi na ilisema kwamba itatoa kwa instalment kila mwaka, basi ifanye juu chini ili Benki yetu ya Maendeleo ya Wakulima iweze kupewa mtaji na wakulima waweze kunufaika na kile ambacho Serikali imewekeza kwenye taasisi.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa, ningependa sana kuwapongeza TANROADS kwenye sekta ya uwekezaji wa SGR, niipongeze sana Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan, Kamati yako ya PAC ilipata fursa ya kuweza kutembelea na kukagua kuangalia uwekezeaji ambao umefanywa wa SGR.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli unaingia kwenye ile treni unasema hivi kweli tupo Tanzania? Hivi kweli Tanzania tumefikia hatua hii? Ni maendeleo makubwa ambayo yamefanyika. Unafika karibu na Kilosa kule unaingia kwenye handaki, kwenye shimo, yaani daraja lipo chini mpaka unasema waoo! Kwa kweli Tanzania tumepiga hatua, nawapongeza sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, kazi hazijasimama, hazijalala, wanachapa kazi. Kwa hiyo niwapongeze sana Serikali kwa kutoa fedha kwa kuwekeza fedha na sisi Watanzania, Wabunge kama Wawakilishi wa Watanzania tunasema kwamba fedha zetu ambazo Serikali imeweza kweli zinafanya kazi, zinaonekana kwa macho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa hii nafasi. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia kwenye bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwanza napenda nimpongeze sana dada yangu Ummy Mwalimu kwa kupata nafasi ya kutumikia katika Wizara hii ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine nimpe pole kwa sababu wizara hii ni wizara ambayo imebeba wizara nyingine nyingi. Elimu ipo kule, afya ipo kule, kilimo kipo kule, kila kitu kipo kule, lakini naamini kwa jinsi ambavyo anafanya kazi, anachapa kazi pamoja na timu yote ya TAMISEMI naamini Insha’Allah Mwenyezi Mungu atamsaidia kama alivyofanya vizuri kwenye Wizara ya Afya, basi na TAMISEMI atafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika bajeti iliyopita nimeona kwamba Wizara ya TAMISEMI iliidhinishiwa jumla ya trillion 5.26, lakini fedha ambayo ilitolewa mpaka inafika Februari, 2021 ilikuwa ni trillion 2.92. Ukiangalia ukubwa na majukumu makubwa ya Wizara ya TAMISEMI kwa fedha hii ambayo ni sawa na asilimia 39.8 haitoshi kukidhi yale yote tumeyazungumza mahali hapa. Waheshimiwa wengi wanalalamika kuhusu maboma wanasema kuhusu miundombinu ya vituo vya afya, miundombinu ya TARURA kwa kweli kwa kiasi hiki cha fedha hakitoshi kukidhi yale ambayo tunayatamani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana kuna Mbunge mmoja alichangia akasema ikiwezekana iletwe kanuni humu Bungeni au sheria ya kuishinikiza mamlaka inayohusika kutoa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo, itoe kadri ambavyo tumepanga.

Mheshimiwa Spika, katika sekta ya afya tumeona Wizara imejitahidi sana hospitali nyingi zimejengwa takribani 99 katika halmashauri lakini vituo vya afya 487, Hospitali za Kikanda tatu lakini haitoshi zahanati takribani 1,198. Pamoja na kujenga vituo hivyo lakini mahitaji bado ni makubwa sana ukilinganisha na jiografia ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika hospitali ambazo zimejengwa au zimekwishajengwa bado kuna changamoto ambazo zinajitokeza, miundombinu bado haijakamilika. Hiyo haitoshi, bado wafanyakazi, kwa sababu huwezi kujenga Hospitali ukaacha kupeleka watenda kazi. Kwa mfano, katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga tuna hospitali ambayo kimsingi haijakamilika bado inafanya huduma za OPD, lakini bado tuna maboma ya vituo vya afya na zahanati 42 ambayo mpaka leo hii hayajakamilika, mengine yameanza kujengwa toka mwaka 2012, 2013 na 2014, mpaka sasa hivi hayajakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nadhani katika bajeti hii na natamani sana nisitoe shilingi ya Waziri kuhusu haya masuala ya kumalizia majengo ya maboma. Yale maboma yana muda mrefu kama Butini kule, Kuni na sehemu zingine nyingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Sinyanga, hayajakamilika kwa muda mrefu. Tuliwahamasisha wananchi wetu, wakajitolea nguvu zao wakajenga yale maboma, lakini yamefika kwenye lenta mpaka sasa hivi bado hayajakamilika. Basi naomba katika bajeti hii inayokuja Serikali ione umuhimu wa kuweza kumalizia maboma haya na kuweza kuwatia nguvu wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kujenga vituo vya afya, hospitali, zahanati na kuweka miundombinu tuna wafanyakazi ambao tunawahitaji katika maeneo yale. Hata hao wachache waliopo kwa kweli tunahitaji tuwakumbuke kama Serikali. Wafanyakazi wengi madaraja hayapandishwi, wafanyakazi wengi haki zao za kimsingi kama fedha ya likizo,matibabu wengi wao wengine hawapati. Tufike mahali tuangalie tuwape motisha hata ng’ombe unapomkamua maziwa ni lazima umpe mashudu. Wafanyakazi wanafanya kazi katika mazingira magumu sana hasa sekta ya afya pamoja na Walimu wote ambao wanafanya chini ya TAMISEMI. Tunajua mazingira ambayo ni magumu, sehemu zingine hata usafiri haufiki. Sehemu nyingine kutoka Makao Makuu ya Wilaya kwenda kwenye kituo anachofanyia kazi ni karibia km100, 110. Kwa kweli inasikitisha sana unakuta mfanyakazi anafanya kazi peke yake katika zahanati lakini stahili zake anazostahili kuzipata hazipati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwasababu inahusika na wafanyakazi wa Idara ya Afya wengine, inahusika na walimu, inahusika na Watendaji wa Kata, Watendaji wa Vijiji ione utaratibu wa kuwapa maslahi yanayostahili watumishi wetu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana. Ahsante Dkt. Mnzava.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika ni dakika tano tu?

SPIKA: Sasa Mheshimiwa Dunstan L Kitandula

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maliasili ya Utalii. Kwanza nipende kuwapongeza sana Waziri pamoja na Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa jinsi ambavyo wanafanya kazi zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri na Naibu Waziri wamekuwa ni watu wasikivu sana, unapowafuata kwa kitu chochote kinachohusu Wizara yao kwa kweli wanachukua muda kusikiliza. Katika hotuba ya bajeti ya Maliasili na Utalii wametoa vipaumbele; moja ya kipaumbele ni kuratibu mapitio ya sheria, sera, kanuni na kuandaa miongozo mbalimbali inayosimamia Sekta hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa kuna migogoro mingi baina ya hifadhi na wafugaji na kupelekea sehemu zingine wafugaji wanauawa au wananchi wanauawa. Tumesikia katika Wilaya za Kiteto, Longido, Ngorongoro na hata Chemba matukio kama haya yanatokea. Ningeomba Wizara kupitia Wizara ambayo inasimamia wafugaji na inasimamia hifadhi ambayo ni Wizara ya Ardhi. Kwa mtizamo wangu naona kwamba Wizara ya Ardhi ina jukumu kubwa sana la kuhakikisha kwamba maliasili inafuata sheria pamoja na wafugaji na wananchi wengine wanafuata sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi ipo toka kuumbwa kwa dunia, haiongezeki na haitaongezeka lakini sisi wanadamu tunazaliana kila siku iitwayo leo. Kwa maana hiyo mahitaji ya ardhi yanaendelea kukua kwa kasi kubwa sana kutokana na population yetu Watanzania, lakini unakuta kwamba hifadhi alama ambazo zilizowekwa au mipaka ambayo iliwekwa enzi zile za mwaka 1940 na ngapi kule bado zinatumika mpaka leo wakati kuna ongezeko kubwa sana la wanadamu. Kwa maana hiyo basi, Wizara ipitie katika vipaumbele vyake ipitie kuangalia sheria, kurekebisha mipaka, kuwapa nafasi wananchi waweze kutumia hiyo ardhi, kwa sababu idadi ya wananchi inaongezeka kila leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa kuna migongano ya matumizi ya ardhi kwa jamii ya wafugaji kati ya wahifadhi, wawekezaji lakini pamoja na wananchi kwa ujumla. Tunaomba Wizara hii ijaribu kushughulikia kuangalia kwamba inatatua vipi matatizo ambayo yanawapata wafugaji. Solution siyo kuwaua tumesikia kuna hili Shirika la TAWA Pamoja na TFS wanafanya kazi zao vizuri, lakini je ni lazima kutumia nguvu, ni lazima kutumia risasi, ni lazima kutumia bunduki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua sheria zipo, basi tunaomba wafuate sheria. Kama kuna wafugaji, kama kuna wananchi, kama kuna taasisi ambayo imeingia kwenye hifadhi tunaomba sheria zisichukue mkondo wake. Kuna chombo ambacho kinatoa maamuzi kuna mahakama, wasichukue sheria mkononi ya kuwaua. Kuna ambao wanapatikana, kuna ambao wanajulikana wameuawa, kuna ambao hawajulikani, unashangaa watu wamepotea. Naomba sana Wizara ya Maliasili na Utalii ikishirikiana na Wizara ya Ardhi, ikishirikiana na TAMISEMI, ikishirikiana na Wizara ya Mifugo wahakikishe kwamba wanafuata sheria, kanuni na taratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipatia nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Afya. Kwanza niwapongeze sana Waziri pamoja na Naibu Waziri wa Afya na Watendaji wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajikita katika suala zima la miundombinu. Ni dhahiri kwamba Serikali yetu imekuwa ikifanya vizuri sana katika miundombinu ya afya hususani majengo. Ukiangalia katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Msalala kulikuwa hakuna hospitali, lakini Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeweza kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo. Hivi ninavyoongea majengo matatu yanaendelea kukamilika, Serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi huo. Pamoja na kwamba ili hospitali iweze kukamilika majengo yanayohitajika ni 22 hivyo, tutaendelea kuiomba Serikali yetu sikivu iendelee kutenga fedha za kutosha ili kuweza kukamilisha ujenzi wa hospitali hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa masikitiko makubwa sana katika Halmashauri ya Msalala kuna Kituo cha Afya cha Ngaya, kimekamilika mwaka 2018, kina wataalam lakini hakuna vifaa tiba. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Afya pamoja na taasisi ambazo zinahusika ziweze kukamilisha kutoa vifaa tiba ili Kituo cha Afya cha Ngaya kiweze kuhudumia wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza na kumkumbuka sana Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa aliyoifanya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama. Halmashauri ya Manispaa ya Kahama imejenga jengo la OPD kwa fedha za ndani, imekwisha kutumia zaidi ya shilingi bilioni 2.7 na inaendelea na ujenzi na tunategemea kufikia mwezi Juni, jengo la hili liwe limekwishakamilika ambalo litatumia zaidi ya shilingi bilioni 3.2.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, nawapongeza sana viongozi wote wa Halmashauri ya Manispaa ya Kahama kwa juhudi kubwa walizofanya kuhakikisha kwamba wanajenga hospitali kubwa ya kisasa kwa kutumia mapato ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka Mheshimiwa Waziri wa Afya aliahidi mbele ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwamba hospitali ile itapandishwa hadhi iwe na hadhi ya hospitali ya mkoa kutokana na kwamba inatibu watu wengi sana kutoka kwenye Wilaya mbalimbali ikiwemo Urambo na Wilaya za Kigoma zote zinakuja Kahama. Hospitali ya Kahama wagonjwa wa nje (outpatient) kila siku wana-attend wagonjwa 800-1,000. Kama hiyo haitoshi, Hospitali ya Kahama ina vitanda 218 lakini wagonjwa wanaolazwa kila siku kwenye ni zaidi ya 300. Kwa hiyo, bado tuna upungufu mkubwa sana wa vitanda katika Hospitali ya Manispaa ya Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiaangalia kwa muundo wa Halmashauri ya Hospitali ya Wilaya ya Kahama, kwa ikama inaonekana watumishi wanatosha, lakini kwa uhalisia idadi ya watumishi hospitali ya Kahama hawatoshi. Kwa sababu ya hiyo takwimu niliyoitoa kwamba wana-attend wagonjwa wengi kwa siku kuanzia 800 mpaka 1,000, lakini wanalaza wagonjwa wengi na vitanda ni vichache. Kwa hiyo, bado tunahitaji watumishi wa kutosha kukidhi mahitaji ya Hospitali ya Wilaya ya Kahama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa mama na mtoto, Hospitali ya Kahama ina vitanda 18 vya kujifungulia wanawake, lakini kwa siku wanawake wanaojifungua katika Hospitali ya Kahama ni 35 mpaka 55. Tunaona jinsi ambavyo kuna uhitaji mkubwa wa kuboresha miundombinu katika hospitali ya Kahama.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke Kahama ipo barabara kuu ya kwenda Burundi na kwenda mikoa mingine ya Geita; Kagera pamoja na Kigoma. Pale pana msongamano mkubwa sana wa watu. Kwa hiyo, inachukua idadi kubwa sana kuhudumia watu wengi kutoka sehemu nyingine mbalimbali. Kwa hiyo, napenda Wizara ya Afya iiangalie Hospitali ya Manispaa ya Kahama kwa jicho la kipekee kutokana na idadi ya watu wengi waliopo mahali pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazidi kuipongeza Serikali na kukumbusha kwamba kuna ahadi ilitolewa na Mheshimiwa Rais ya shilingi milioni 500 kama mwanzo wa kununua vifaa tiba. Tunaomba fedha hiyo Serikali yetu sikivu iweze kutoa ili wananchi wa Wilaya ya Kahama waweze kupata vifaa tiba na hospitali iweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaipongeza Serikali, kwa kweli imeweza kujenga vituo vya afya kama Mwendakulima, Nyasubi, kuna waganga, kuna waunguzi, lakini tatizo linarudi pale pale kwenye vifaa tiba. Tunaomba sana vifaa tiba viweze kutolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo haitoshi, katika Halmshauri ya Wilaya ya Kishapu, tuna Kituo cha Afya cha Nobola cha toka enzi za Mwalimu. Kituo kile kinahudumia Kata tisa na pembeni yake hakuna kituo kingine chochote cha afya. Vile vile kutoka pale Nobola kwenye Makao Makuu ya Wilaya ni zaidi ya kilometa 40 mpaka 50. Naiomba Serikali iweze kuboresha na kujenga kituo cha afya kingine katika Kata nyingine aidha Talaga au Lagana ili wananchi wa Wilaya ya Kishapu nao waweze kupata huduma ya afya kwa usahihi na kwa manufaa mazima ya afya zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini, kuna Health center ambazo zimejengwa vizuri, tunamshukuru Mwenyezi Mungu, tunawashukuru wataalam wetu na tunaishukuru Serikali kwa kutukumbuka watu wa Shinyanga. Kituo cha Afya Samuye pamoja na Tinde vinafanya kazi. Tinde kinafanya kazi vizuri sana, lakini Samuye kimejengwa, kina theatre, kina wafanyakazi, lakini hakuna vifaa, huu ni mwaka wa tatu sasa. Kwa hiyo, tunaona Serikali iweze kukukumba.

Mheshimiwa Naibuy Spika, kuna wananchi wa Kata ya Solwa, wamejenga kituo cha afya kwa nguvu zao, kuna wodi mbili wameshajenga, kuna OPD nzuri, lakini kupandishwa hadhi kutoka kwenye zahanati kuwa kituo cha afya bado Wizara inasuasua. Tunaomba mwafikirie wananchi hawa ambao wametumia fedha zao nyingi kujenga miundombinu hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nitapenda kuzungumzia suala la magonjwa yasiyoambukiza. Kumekuwa kuna mlipuko wa magonjwa yasiyoambukiza kwa wananchi, mengi sana. Mfano, kisukari, magonjwa ya moyo na magonjwa mengine, lakini afua ambazo zinatekeleza intervention hizo zimekuwa zikisuasua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana Wizara ya Afya kupitia Kitengo cha Tiba Mbadala. Tunaomba sasa dawa ambazo zinagundulika kwamba zinafanya kazi, ziweze kutolewa kwa bei nafuu, ziweze kupewa vibali ambavyo vinastahiki. Mfano hiyo Phyt Exponent, tunaomba hiyo dawa iweze kupunguziwa masharti, iweze kupunguziwa masharti, iweze kusajiliwa kama dawa ya tiba mbadala kuliko kuwa na Dietary supplement. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutumia fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Mapendekezo na Mwongozo wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kujikita katika maeneo mawili ambayo ninafikiria ni vizuri na mimi nikatoa mchango wangu, nipende kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia, kwa kazi kubwa anayoifanya kuhakikisha kwamba anatuletea maendeleo na kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona hivi karibuni amekuwa akisafiri huku na huku kuhakikisha kwamba Watanzania tunaendelea kunufaika na mambo yote mazuri ambayo yako duniani, hasa katika suala zima la janga ambalo lilikuwa limetupata la UVIKO-19. Tumeona ni jinsi gani ambavyo ameweza kutafuta fedha na kupata zaidi ya trilioni 1.3 kwa ajili ya kupambana na UVIKO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hakuishia hapo, alifikiria mbele zaidi akaona fedha hizi ni vizuri kuzipeleka kule ambako ndiyo kuna chanzo cha tatizo. Zimekwenda kujenga shule, kupunguza msongamano, lakini zinakwenda kujenga vituo vya afya kuhakikisha kwamba huduma zote za kukabiliana na UVIKO-19 zinaimarika. Haitoshi, tunajua chanzo na njia moja wapo ya kujikinga na UVIKO ni kunawa mikono, ameimarisha mfumo mzima kupeleka fedha kwa ajili ya kupata maji safi na salama. Kwa hiyo, ninampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujikita katika suala zima la kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu. Uchumi bila viwanda haiwezekani, itakuwa ni ndoto. Ninapongeza sana Wizara kwa kuona kipengele hiki kuhakikisha kwamba inajenga uchumi shindani na maendeleo kwa watu. Lakini maendeleo kwa watu hayawezi yakaja kama viwanda vyetu nchini haviongezeki au vilivyopo havifanyi kazi kwa tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Shinyanga kuna kiwanda cha nyama kimejengwa mwaka 1951. Toka kilipojengwa hakijawahi kuzalisha hata kilo mbili za nyama, kina eneo kubwa sana la uwekezaji, Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kwamba inaomba lile eneo kwa ajili ya kutengeneza mazingira ya uwekezaji, kuwavutia wawekezaji wengine ambao wanahitaji kuja katika Mkoa ule kuwekeza ili waweze kupata ardhi na kuweza kujenga viwanda vingine au kuboresha kiwanda kilichopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo ni kwamba lile eneo la kiwanda cha nyama liko chini ya Wizara ya Mifugo pamoja na Wizara ya Fedha. Tumekuwa tuki-struggle sana tuweze kupata lile eneo ili wanapokuja wawekezaji Mkoa wa Shinyanga ardhi ipatikane bure, wenyewe waweze kujenga viwanda, waweze kulipa kodi, lakini waweze kuajiri vijana ambao ni vijana wengi sana hawana ajira sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imefanyika Kahama, kulikuwa kuna eneo Kahama linaitwa Zogomela, lina hekta zaidi ya 2,000. Halmashauri iliomba Wizara ya Mifugo – lilikuwa eneo la Wizara ya Mifugo, likatolewa kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, wameweza kuweka uwekezaji. Sasa hivi mwekezaji anapofika Tanzania akitaka kuja kuwekeza katika baadhi ya Halmashauri ambazo zina fursa ya kuwekeza moja wapo ni Kahama, mwekezaji anapewa ardhi, anajenga kiwanda, analipa kodi zote za Serikali za ardhi na kadhalika lakini anazalisha ajira nyingi kwa wazawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Wizara ya Mifugo na Wizara ya Fedha zisitoe lile eneo ambalo liko Tanganyika Packers pale Shinyanga na eneo lingine la Chibe ambalo lina zaidi ya hekta 8,000, limekaa tu halina kazi, Wawekezaji wanapokuja wakitaka ardhi kwenda kulipa fidia kwa wananchi wa kawaida inakuwa ni gharama kubwa sana. Anaangalia mkoa mwingine ambao una fursa ya ardhi ambayo haina masharti makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ninaomba katika suala zima la kutaka kuhakikisha kwamba uwekezaji wa viwanda kwa maendeleo ya watu tuangalie na maeneo ambayo tuna ardhi kubwa, iko chini ya Serikali, wawekezaji wanakuja wanahitaji kupata lile eneo ili waweze kuwekeza, basi kusiwe na milolongo mingi ya kuweza kutoa lile eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuzungumzia kuhusu suala zima la kilimo. Kila Mbunge anayesimama hapa anaongea kuhusu suala la kilimo, na wengine wataendelea kuchangia sekta ya kilimo kwa sababu ndiyo uti wa mgongo. Suala zima la kilimo tumeona kabisa kwamba katika mpango huu sekta ya kilimo inachangia Pato la Taifa kwa zaidi ya asilimia 26, lakini huu ni ule ulimaji wa kawaida wa kutegemea mvua, na tumeshaambiwa kabisa mwaka huu mvua zinaweza zikawa siyo nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali Tanzania tunajipangaje kwa mpango wa muda mrefu kuhakikisha kwamba nasi tunabadilika kama nchi ya Israel ilivyobadilika, kama jinsi ambavyo Dubai imebadilika. Nchi zile ni majangwa lakini wameweza kuhakikisha kwamba wanaboresha kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huku kwenu Kongwa huku, kipindi cha masika kuna maji yanapotea hovyo, ukishavuka sehemu moja ya Chamwino huku kama unakwenda Dar es Salaam masika maji yanajaa sana mpaka magari yanachukuliwa na maji.

Ukienda Bahi Road huku kama unakwenda Shinyanga kuna eneo pale la Bahi, maji yanajaa mpaka yanapotea, Serikali ije na mpango wa kuhakikisha kwamba na sisi tufike hatua Tanzania tuweze kuvuna maji. Mbona nchi nyingine wameweza? Hawakuanza mara moja, ni mpango wa muda mrefu, ni ambao unatumia fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tufikirie sasa kwamba kwa miaka ijayo tuhakikishe kwamba tunatafuta fedha za kuweza kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji ili sasa tutoke pale kwenye Pato la Taifa la asilimia 26 tuweze kwenda juu. Tumeona kabisa kwamba kuna uhitaji lakini mbali na suala zima la umwagiliaji bado kuna tatizo la bei kubwa za pembejeo.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipatia nafasi na mimi kuweza kuchangia katika hoja ambazo zimewasilishwa, nitakwenda kujikita kuchangia katika hoja iliyowasilishwa na Kamati ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma. Tumeona katika taarifa iliyotolewa kuna baadhi ya changamoto ambazo zinakabili haya Mashirika ya Umma ambayo yamewekeza. Katika changamoto mojawapo ni Taasisi kutofanya kazi kwa pamoja kumekuwa na sintofahamu ya Taasisi mbili za Serikali, ambazo moja imewekeza lakini moja inasaidia nyingine kuweza kufanya kazi kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano kuna Shirika la TANESCO pamoja na STAMICO. STAMICO tunajua kwamba ni Shirika la Serikali na limewekeza zaidi ya asilimia 99 ya mtaji na katika ndani ya Shirika la STAMICO, kuna Stamigold ambao wana kiwanda cha madini Biharamulo. Tatizo ambalo linatokea ni kwamba Stamigold ili kuendesha shughuli zake linahitaji umeme mkubwa sana karibia unit 1,300,000. Lakini tatizo lililopo ni kwamba Stamigold hawajaunganishwa na grid ya Taifa wanajikuta kwa mwezi, gharama ya kuendesha mitambo na gharama ya uchimbaji na uchenjuaji inatumia zaidi ya shilingi bilioni 1.5 kununua mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama TANESCO wangeweza kuwaunganishia umeme grid ya Taifa, wangeweza kuokoa takribani shilingi bilioni 8 kwa mwaka kwa gharama ya mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunavyojua kwa sasa hivi lita ya mafuta ya dizeli ni Shilingi 2,500/= Stamigold wanatumia zaidi ya lita 600,000, kwa mwezi kwa ajili ya kuendesha mitambo na kwa ajili ya kufua umeme ili waweze kufanya kazi zao. Sasa basi, kama kunakuwa kuna mahusiano mazuri ya Taasisi mbili za Serikali ambazo zina lengo moja kuhakikisha kwamba, Tanzania yetu inakuwa na uchumi imara TANESCO wangefanya juhudi za makusudi kuhakikisha kwamba wamewaunganishia umeme kwa grid ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imeshafuatilia sana lakini hata STAMICO wameshafuatilia sana suala hili. Mkienda maeneo ya tukio mkienda kwenye ule mgodi wakisikia Kamati inakwenda ndio mnakuta TANESCO, wameanza kuweka vifaa vyao wamechimba kama futi 2 tu mkiondoka shughuli inasimama sasa tatizo ni nini? Kwa sababu, Mashirika mawili ya Umma yanapofanya kazi pamoja tija na ufanisi vinaonekana dhahiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Taasisi za Serikali ambazo zinategemeana kwa namna moja ama nyingine zihakikishe kwamba, kunapokuwa kuna uhitaji wa Shirika la STAMICO/Stamigold wanahitaji TANESCO ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi basi; ni vizuri Taasisi/mamlaka ambazo zinahusika kuhakikisha kwamba wanasaidia/wanawezesha Shirika moja kufanya kazi zao kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kabisa kwamba kunapokuwa na gharama kubwa za uendeshaji faida inakuwa kidogo. Kwa mwaka 2019/2020 STAMICO iliweza kutoa gawio la shilingi bilioni 1.1 kwa maana hiyo basi kama uendeshaji utapungua kwa kuwa na umeme wa uhakika, kutoka kwenye grid ya Taifa ni dhahiri kwamba hata gawio la Serikali litaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama STAMICO/ Stamigold wanatumia gharama kubwa au Shirika lingine lolote lile linatumia gharama kubwa kwenye uendeshaji, ni dhahiri kwamba lazima itapata hasara. Kwa sababu matumizi ya uendeshaji yanakuwa juu sana kwa hiyo, niwaombe sana sana sana Taasisi kutimiza wajibu wake kurahisisha utekelezaji wa Mashirika mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kuweza kunipa nafasi ili na mimi nichangie katika bajeti iliyopo mbele yetu. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa wasilisho lake la jana kwa bajeti ambayo kwa kweli inatupeleka tunapotaka.

Mheshimiwa Spika, ninaishukuru sana Serikali kwa kuongeza kiwango cha bajeti, na kwa hivyo nitazungumzia katika masuala mazima ya kuzuia maambukizi ya UKIMWI. Kwa kipindi cha mwaka 2022/2023 Serikali imetenga zaidi ya bilioni 1.8 kwa ajili ya kutekeleza afua za kupambana na maambukizi ya UKIMWI. Hata hivyo nitoe masikitiko yangu kwa bajeti hii ambayo inakwenda kumalizika mwezi wa sita, Serikali ilitenga kutoa Shilingi bilioni moja kwa afua za kupambana na maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwa fedha za maendeleo zinazotokana na mfuko wa ndani.

Mheshimiwa Spika, wafadhili au fedha za nje zilikuwa jumla ya milioni mia tatu themanini na kitu, na wafadhili wametoa fedha kwa asilimia mia moja. Hata hivyo, lakini kwa masikitiko makubwa fedha za ndani ambayo ni milioni moja ilitengwa mpaka Machi haikutoka hata Shilingi moja. Sasa nikifikiria juhudi ambazo tunazo kama nchi na malengo ya Dunia ya kudhibiti maambukizi mapya virusi vya UKIMWI; na Tanzania tukiwa katika mstari wa mbele kuhakikisha kwamba maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI, yanapungua. Sasa kama bajeti ya Serikali, vyanzo vya ndani fedha hazitoki, ikitokea wafadhili wameacha kutoa fedha itakuwaje? Napata mashaka sana napata uchungu sana.

Mheshimiwa Spika, tunajua kwamba kuna mkakati wa kufikisha asilimia 95 ya watu wote ambao wanapimwa virusi vya UKIMWI kujua afya zao, asilimia 95 kwa wale ambao wamegundulika na virusi vya UKIMWI kuhakikisha kwamba wanakuwa katika matibabu; na asilimia 95 ya wale ambao wapo kwenye matibabu kuhakikisha kwamba wanapima kujua wingi wa virusi. Sasa kwa trend hii ya utoaji fedha, napata mashaka.

Mheshimiwa Spika, suala la maambukizi ya UKIMWI naona bado ni tatizo kubwa, hasa kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15 mpaka 24. Vile vile kwa wananchi ambao wapo pembezoni; wako kwenye mialo, maeneo ya migodi, hasa sasa hivi kumekuwa kukizuka migodi mingi. Mfano Mkoa wa Shinyanga, maeneo ya Kahama, Mwakitolio kuna migodi mingi ambayo inaibuka. Sasa hali ya kiafya, hali ya kuzuia maambukizi ya virusi vya UKIMWI imekaaje.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya Takwimu ya Tanzania HIV Impact Survey iliyofanyika mwaka 2016/2017 inaonesha kwamba idadi ya vijana wengi wenye umri wa miaka 15 mpaka 24 wameshajiingiza katika vitendo vya kujamiiana. Katika idadi hiyo ya kundi hilo hilo la hao vijana wa miaka 20 hadi 24, kati yao wasichana wameambukizwa zaidi kwa asilimia 3.4 ukilinganisha na wavulana ambao wameathirika, wameambukizwa kwa asilimia 1.9. Hii inaashirika nini? Ni kwamba vijana wetu wengi wameshaingia katika hili janga la maambuziki ya virusi vya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, fedha ambazo zinatolewa na Serikali, fedha za ndani hazitolewi kwa wakati. Tunategemea kwa asilimia kubwa wafadhili. Je, tutawalinda hawa vijana ambao kwa kweli wapo kwenye risk kubwa? Je, tutawafikia wale watu ambao wapo kwenye mialo? Kwa tabia za wavuvi, wanaondoka majumbani kwao usiku kwenda kutega, wanarudi alfajiri wamechoka. Inabidi sisi watoa huduma za afya ndio tufanye juhudi binafsi kuwafuata kuwafikia.

Mheshimiwa Spika, kwa trend ya fedha ambazo zinatengwa na Serikali tunapitisha hapa Bungeni, lakini hazitoki kwenda kuwahudumia au kuwafikia kule. Kwa kweli bado ninaona suala zima la vita dhidi ya maambukizi mapya ya UKIMWI itakuwa ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, ukiangalia hata katika hii tafiti ya vijana iliyofanyika, wanaopima wengi ni wasichana; wavulana hawapimi. Kwa nini? Kwa sababu baba zao wenyewe hawapimi; na ukizingatia kwamba malezi yanaanzia nyumbani. Baba hana interest ya kupima, anasubiria mke wake awe mjamzito, aende akapime kliniki, akishagundulika kwamba yupo salama, basi naye anajiaminisha kwamba yupo salama. Hakumbuki kwamba kuna maambukizi ambayo mwenza mmoja anaweza akawa na maambukizi na mwingine asiwe na maambukizi, unaona.

Mheshimiwa Spika, kama baba hana utamaduni wa kwenda kupima, huyu kijana wa kiume atakuwa na courage ya kwenda kupima? Jibu ni hapana. Niwasihi sana wanaume, mjitokeze kwenda kupima, kwa sababu ninyi ndio mnaowafuata hata hao wasichana wadogo wenye miaka 20 mpaka 24, ambao wako Vyuo Vikuu, kwenda kuwarubuni, kuwapa vichipsi mayai, kuwanunulia vi-IST, ili mwarubuni wapate UKIMWI ambao tayari wanao. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba anachokizungumza kwamba wanaume hatuna tabia za kupima, siyo kweli. Wanaume tuna tabia za kupima; na hata Wabunge wanaume hapa ndani tupo tayari kwenda kupima afya zetu hapo nje. (Makofi)

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, siIkubali hiyo taarifa kwa sababu utafiti ndivyo unavyoonesha. Ameshasema kabisa kwamba leo nje pale atakwenda kupima, kwa maana hiyo, hajapima mpaka sasa hivi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba wanaume wengi hawapimi na wana tabia ya kufuata watoto wa shule ambao wana miaka 20 mpaka 24, lakini hata sasa hivi na sisi wanawake kuna wimbi ambalo limetokea, wanawake wengi hasa wenye uwezo wa kipato kuwarubuni watoto wetu wa kiume na kwenda kuwaambukiza virusi vya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe shime kwa Serikali yetu chini ya Wizara yetu inashughulikia masuala ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwamba tunahitaji nguvu ya ziada kuhakikisha kwamba tunaelimisha watoto wetu, vijana wetu ambao wapo shule za sekondari na vyuo vikuu kwamba UKIMWI bado upo, ni janga kubwa sana la kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la maambukizi mapya ya UKIMWI. Tumekuwa kwenye ziara Kanda ya Ziwa. Kwa kweli maambukizi ya virusi vya UKIMWI bado yapo juu, hasa katika Mkoa wa Mwanza. Kwa survey iliyofanyika mwaka 2016/2017, maambukizi ya UKIMWI yametoka kutoka kwenye asilimia 4.7 kwenda 7.2 ambapo ukilinganisha na ya kitaifa ambayo ni 4.7 unaona kabisa bado kuna maambukizi mapya yanayokuja kwa kasi kwenye mikoa ya Kanda ya Ziwa. Hii ni kwa sababu kuna highways, kuna mipaka, kuna migodi mingi, kuna wavuvi na mialo. Kwa hiyo, kuna mazingira hatarishi ambayo yanapelekea wananchi wetu kupata virusi vya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, hiyo, naomba basi, kwa bajeti hii ambayo tunakwenda kuipitisha, kwenye masuala mazima ya kupambana na virusi vya UKIMWI, kama Serikali imetenga shilingi bilioni 1.8 kwa fedha za maendeleo za ndani tunaomba izitoe hizo fedha ili afua ambazo zinatolewa ziweze kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, napenda kusema kwamba UKIMWI upo, UKIMWI unaoua. Pamoja na kwamba sasa hivi tunajielekeza kwenye magonjwa yasiyoambukiza, kweli yapo na yanatusumbua wengi, hasa Wabunge kwa sababu muda mwingi tunakaa, wengine hatutaki kufanya mazoezi, tunakula vizuri; naomba kabisa kwamba juhudi ziongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, magonjwa yasiyoambukiza ni hatari kushinda UKIMWI, kwa sababu ukiugua Kisukari hapa, ukiugua Hypertension na masharti ya vyakula yanabadilika, lakini UKIMWI utakula kila kitu. Kwa hiyo, magonjwa yote yanayoambukiza na yasiyoambukiza ni lazima tupambane nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema kwa kuendelea kutupa uhai na afya njema, na leo amenipa kibali cha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita ya mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo inafanyika katika Wizara hii ya Maji. Nawashukuru sana Waziri na Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote. Kwa kweli mnafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi wa Ziwa Victoria ulianza katika Mkoa wa Shinyanga, ukijumuisha Mkoa wa Shinyanga Mjini pamoja na Manispaa ya Kahama. Kwa kweli sisi wakazi wa Shinyanga ambao tulizaliwa miaka ya 1970 tukakulia pale Shinyanga, tunajua adha ambayo tulikuwa tunaipata. Ilikuwa kabla hujaenda shule, ni lazima uhakikishe umechota maji, na unayachota saa nane usiku, ndiyo unaweza ukayapata yakitoka kwenye Bwawa la Lilwa; lakini sasa hivi maji katika Mkoa wa Shinyanga hasa Shinyanga Mjini na Kahama ni historia. Tunaishukuru sana Serikali yetu kwa juhudi kubwa ambazo imezifanya.

Mheshimiwa Spika, Shinyanga ina majimbo sita. Jimbo la Ushetu lipo katika Wilaya ya Kahama, lakini ni Jimbo pekee ambalo maji ya Ziwa Victoria hayajafika. Ukitoka Kahama kwenda Tabora ni kilomita nyingi, lakini kutoka Kahama Mjini kwenda Ushetu, Kijiji cha mwisho cha Manispaa ya Kahama kwenda Ushetu ni kilomita tano; kutoka Nyandekwa kwenda Ukune ni kilomita tano; kutoka Nyandekwa kwenda Igunda ni kilomita saba; lakini watu wao hawana maji. Mheshimiwa Aweso mmefanya kazi kubwa sana, na tunashukuru katika bajeti hii mmeweza kusema kwamba mmetenga Shilingi bilioni 47 kwa ajili ya maji ya Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu. Tunaomba tutakapopitisha bajeti hii, masuala ya upembuzi yakinifu, usanifu, yafanyike kwa haraka ili wananchi wa Ushetu nao waweze kuepukana na hii adha ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia maji yamefika Tabora. Kutoka Ushetu kwenda Kaliua, ni kilometa kama 40. Kule Tabora wenzetu wanapata maji, huku Ushetu hawapati maji. Wale wananchi wanakuwa wanyonge, wanaanza kuwaza vibaya kwamba kwa nini sisi tumetengwa? Mheshimiwa Waziri kwa sababu kwenye bajeti hii mmetenga fedha shilingi bilioni 47 kwa ajili ya Halmashauri ya Ushetu, tunaomba basi mweze kutekeleza suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru sana kwa Halmashauri ya Msalala, maji ya Ziwa Victoria katika baadhi ya Kata yapo, hasa katika ule mradi wa upanuzi wa maji ya Kagongwa – Isaka. Tunashukuru sana, matenki matatu yenye ujazo mkubwa wa lita 470,000, yameshajengwa, na utekelezaji umefikia asilimia 80. Kuna vijiji ambavyo vinafaidika kama Jana, Mwalugulu na Itogwamholo, tunaomba basi, katika Halmashauri ya Msalala, kata ambazo hazijafikiwa na haya maji, waweze kupata maji. Ukiangalia Ikinda kule, maji hayajafika; ukiangalia Lunguya, maji hayajafika. Tunaomba kuwe na usawa ili kila mtu aweze kufaidi haya maji ya Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata katika Jimbo la Kishapu, Wilaya yetu ya Kishapu kuna miradi ambayo inaendelea. Kuna utekelezaji wa mradi ambao unatokea Kishapu – Mwataga, Mkandarasi tayari yuko kazini. Tunaomba huyo Mkandarasi aanze kazi mara moja. Speed aliyonayo Mheshimiwa Waziri, tunaomba na kwa watendaji speed hiyo hiyo iendelee.

Mheshimiwa Spika, pia tumepata mradi wa Shilingi bilioni 6.5 wa Igaga - Mwamashele - Ngofia – Lagana, na Mkandarasi yuko site. Tuseme nini sisi watu wa Shinyanga? Kwa kweli tunashukuru. Kwa sababu upungufu ni kidogo kuliko mafanikio na maendeleo ambayo tumeyapata kwenye sekta hii ya maji. Tunaomba basi sehemu ambapo kuna upungufu, Serikali iongeze msukumo. Watu wa SHUWASA, DUWASA na RUWASA, wanafanya kazi kubwa sana, wanatusikiliza Wawakilishi wa Wananchi, wanafanya mambo makubwa sana, na Waheshimiwa Waheshimiwa wa Majimbo wanapambana sana kuhakikisha kwamba wananchi wao wanapata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie na Jimbo la Solwa, Wilaya ya Shinyanga. Kwa kweli katika Wilaya hii, nafikiri kama kuna Wilaya ambazo zimependelewa, na Mheshimiwa Mbunge ame-fight sana kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata maji, basi ni katika Jimbo la Solwa. Kwa kweli kuna miradi mikubwa ambayo inaendelea; mradi wa Tinde – Shelui, zaidi ya vijiji 34 vinapata maji, vikiwemo 22 vya Jimbo la Solwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, tunaomba basi utekelezaji wa sehemu ambazo maji hayajafika hasa katika miradi ambayo inaendelea na fedha zimekwisha tengwa basi maji yaweze kufika kwa wakati na wananchi wa Mkoa wa Shinyanga hususani Jimbo la Solwa, waendelee kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba nitoe ushauri, Serikali yetu imetenga fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maji, wakandarasi wako site, wengine wanakaribia kumaliza kazi zao, wengine wamekwisha maliza. Tunaomba muwalipe fedha kwa wakati kusiwe na ucheleweshaji wa aina yoyote. Kwa sababu unapomchelewesha mkandarasi kuna masuala mazima ya kupigwa faini.

SPIKA: Mheshimiwa Christina, kengele ya pili imeshagonga ahsante sana.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ninaunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Wizara ya Afya. Kwanza nimshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na uwekezaji mkubwa ambao ameufanya katika Wizara hii ya Afya kwa kujenga miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba takriban Tanzania nzima, kila wilaya kuna kazi ambayo inaendelea kwa sasa hivi. Kama siyo jengo la OPD basi jengo la MD kama siyo wodi basi ni zahanati; yaani kila sehemu kuna kazi ambayo inaendelea. Kwa kweli nampongeza sana Mheshimiwa Rais, lakini nawapaongeza sana sana sana Wizara ya Afya chini ya Mama yetu Ummy Mwalimu pamoja Doctor Mollel nadhani Ummy pamoja na Mollel hawalali katika kuhakikisha kwamba Wizara ya Afya inasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni shahidi watumishi wa Wizara ya Afya wanafanya kazi nzuri nzuri sana iliyotukuka; kwa nini nasema hivyo? Ukienda kwenye hospitali zetu kwa sasa, kwa mfano mimi nitatolea mfano wa Hospitali ya Benjamin Mkapa; wanafanya kazi nzuri wanahudumia vizuri, yaani wanatibu kwa weledi. Lakini tatizo liliopo kwa sisi Watanzania ambao hatuna bima ya afya ni changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa si muumini sana wa ile bima kwa wote. Sasa hivi kutokana na gharama za matibabu, hasa kwa wagonjwa ambao wana matatizo makubwa kwa kweli bima kwa wote inahitajika. Usipokuwa na fedha ni ngumu sana mgonjwa wako akapata huduma inayostahili. Kweli atapokelewa na atahudumiwa, lakini kuna vipimo ambavyo vinahitajika kuna dawa ambazo zinahitajika, ni lazima uingie mfukoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa ninawaza je, yule mama wa kijijinim jem yule baba wa kijijini ambaye ni mkulima na hana kipato cha kutosha anapopata matatizo makubwa kwenye familia yake anafanya nini? Ninaomba sana suala la bima kwa wote mlilete mapema Bungeni ili tuweze kulijadili na kulipitisha kwa sababu ni Watanzania wengi ambao wanahitaji…

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nampa taarifa mzungumzaji kwamba suala la Bima ya Afya ni muhimu. Mimi kwa upande wa Ushetu wakulima wangu wote 800 walijiunga na ushirika wa afya, na wanasisitiza hili suala liletwe Bungeni lipitishwe haraka ili wakulima wa-enjoy na ushirika wa afya. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa taarifa hiyo.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa ya kaka yangu Cherehani, ni kweli tuna haja ya kuletewa huo mpango wa bima ya afya kwa wote kwa sababu ni Watanzania wengi sana ambao wanahitaji huduma ni Watanzania wengi sana ambao hawana uwezo wa kwenda hospitali na kulipia matibabu kwa pesa taslimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru tena Serikali kwa kutenga bajeti ya Wizara hii ya Afya na kuweza kuongeza bajeti kutoka bilioni 1.1 mwaka jana ya bajeti inayomalizika na mwaka huu wameweza kutengewa fedha bilioni 1.2 na kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli tuna haja sana ya kuipitisha Bajeti ya Wizara ya Afya, kwa sababu bila afya hatuwezi kukaa mahali hapa. Bila afya hatuwezi kufanya kitu chochote. Kwa hiyo afya ni msingi lakini kwenye taarifa ya Wizara ya Afya kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi. Ukiangalia mahitaji ya watumishi katika zahanati zetu Tanzania nzima ni 100,646, waliopo ni 30,625 upungufu ni 70,000 sawa na asilimia 70, upungufu wa watumishi katika zahanati, lakini kwenye vituo vya afya mahitaji ni watumishi 68,204, waliopo ni 25,354, upungufu ni 42,850, sawa na asilimia 73. Kwenye hospitali za wilaya wanaohitajika ni 123,424, waliopo 29,409, upungufu ni asilimia 94,215, sawa na asilimia 76.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ina maana gani? Kama kuna upungufu mkubwa wa wafanyakazi kiuhalisia hata huduma hazitakuwa bora. Kwa sababu, kuna kiwango ambacho mtoa huduma za afya anatakiwa ahudumie, kuna viwango ambavyo vimewekwa na Wizara ya Afya. Sasa ukiangalia kwa upungufu huu wa asilimia 70, asilimia 63, asilimia 76 ni uhalisia kwamba watumishi hawa wanafanyakazi kupita kiasi na mtu anapofanyakazi kupita kiasi, matokeo yake atachoka, kwa sababu ni mwanadamu. Matokeo yake ataanza kutoa huduma ambayo sio bora, anaweza akaghafilika, ndio maana unakuta kuna sehemu zingine kuna watumishi ambao wanatoa lugha chafu, sio kwamba amedhamiria kutoa ile lugha chafu ni kwa sababu kazi zimemzidia amechoka, anajikuta anajibu kitu ambacho hakupanga kukijibu. Tunaiomba sana Serikali katika ajira ambazo zinatolewa na Serikali, waangalie sana sana sana Sekta ya Afya, kwa sababu ni sekta ambayo inahusu maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama, Hospitali ya Wilaya ya Kahama kwa siku inahudumia wagonjwa 450 mpaka 715 OPD na tuna watumishi 396. Pamoja na kwamba ni hospitali ya wilaya lakini inafanya kazi kama hospitali ya mkoa na tumekwenda mbali sana, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama wameweza kujenga majengo kwa kutumia fedha za ndani. Wametumia bilioni za kutosha kujenga OPD, zaidi ya bilioni nne, wamejenga kwa fedha za ndani lakini haikutosha wamejenga jengo la uchunguzi wametumia zaidi ya milioni 803. Wamejenga Kituo cha Afya cha Kagongwa cha thamani ya milioni 800 kwa mapato ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali, halmashauri zinapokusanya mapato yake ya ndani zikajenga miundombinu ya afya, tunaomba kwa haraka mtupe support kuhakikisha kwamba vifaa tiba vinatolewa. Tuna jengo pale pale la uchunguzi lakini hatuna vifaa tiba, Serikali watusaidie tuweze kupata vifaa tiba ili wananchi wa Wilaya ya Kahama waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kahama haihudumii wakazi wa Kahama pekee yake inahudumia Geita, Kaliua, Urambo, Msalala, Nzega, inahudumia watu wanaopita kutoka Tanzania kwenda Burundi. Kwa maana hiyo basi, kwa sababu Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alikwishatamka kwamba Hospitali ya Wilaya ya Kahama iwe na hadhi ya Hospitali ya Mkoa. Tunaomba Wizara ya Afya, huo mchakato ambao wamekwishauanza ukakamilike ili tuweze kupunguza uzito wa huduma ambayo wale wafanyakazi ambao wako katika ikama ya hospitali ya wilaya waweze kuwa katika ikama ya hospitali ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika Wizara ya Afya inafanya kazi kubwa sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Dkt. Mnzava, kengele ya pili hiyo.

MHE. DKT. CHRISTINA P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, tunaomba watusikilize. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Wizara hii. Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutupa afya njema na kibali cha kusimama mahali hapa.

Mheshimiwa Spika, lakini namshukuru sana na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa maono yake makubwa kuanzisha Wizara hii mama ambayo inashughulika na ustawi wa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia katia hotuba ya bajeti ya Wizara hii iliyoko mbele yetu kuna vipaumbele kadha wa kadha ambavyo wameviweka. Moja ya kipaumbele ni kuendelea kuimarisha huduma za ustawi wa jamii na haki kwa familia na watoto ikiwemo malezi ya kambo na kuasili, malezi makuzi na maendeleo ya jamii, lakini zaidi ni kuhakikisha kwamba kunakuwa na maendeleo ya awali, ulinzi na usalama kwa watoto dhidi ya vitendo vya ukatili.

Mheshimiwa Spika, katika nchi yetu hivi karibuni kumekuwa na wimbi kubwa la ukatili wa kijinsia, ukatili wa kingono, ukatili wa kifikra, lakini ukatili wa kimwili. Ukiangalia hasa katika Mkoa wa Shinyanga inaonesha kabisa ni dhahiri kwamba kuna ukatili mkubwa wa kijinsia. Ukiangalia takwimu inaonesha kwamba kutoka Juni, 2020 hadi Disemba, 2021 ukatili wa kingono kwa watu wazima umekuwa na matukio karibia 217; lakini kwa watoto ukatili wa kingono watoto jumla 661 wamefanyiwa ukatili wa kingono. Katika hiyo idadi ya watu wazima 217 ambao ni wanawake kwa wanaume waliyofanyiwa ukatili wa kingono, kesi ambazo zilipelekwa Mahakamani ni 149 kati ya 217 na ambazo zilipelekwa Makamani zikahukumiwa ni kesi 80 peke yake. Hii inasikitisha sana, watu wazima 217 lakini watoto 661, kesi ambazo zimepelekwa Mahakamani ni 149 tu na ambazo zimekuja kuamuliwa kesi 80 hii haikubaliki. Tatizo ni nini, hapa kuna tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jamii yetu imekuwa ikinyanyasika katika ukatili wa kijinsia, ukatili wa kingono, ukatili wa kimwili, lakini ukatili wa kihisia. Kesi zinapelekwa Mahakamani na ukizingatia sheria hii ya watu wanaofanya ukatili hasa la suala zima la wanaobaka, wanaolawiti, wanaofanya vitendo vyovyote vile vya unyanyasaji wa kingono, sheria inampa dhamana mhusika, wakishawekewa dhamana wanatoroka, kesi zinapotelea hewani.

Ningeomba Mheshimiwa Waziri kama inawezekana sheria inawa-favor wale watu ambao wanafanya uhalifu, basi sheria iletwe hapa Bungeni tuweze kurekebisha. Kwa sababu kama mtu anahujumu uchumi, anakuwa hana dhamana, je, anayehujumu uhai wa mtu inakuwaje, hili halikubaliki. Tunajenga kizazi ambacho kinakuwa na maisha magumu, angalia watoto wa mitaani walivyo wengi, ukitafuta historia ya hawa watoto ni wengi ambao wamenyanyasika majumbani na watu ambao wanawanyanyasa hawa watoto au wanawafanyia vitendo vya ukatili ni watu ambao wanatuzunguka, wanaweza wakawa ni ndugu zetu, wanaweza wakawa ni majirani, wanaweza wakawa ni walimu. Lakini anapobainika ya kwamba amefanya ukatili akafikishwa kwenye chombo cha sheria anahaki ya kupata dhamana. Akishapata dhamana, amewekewa dhamana na watu wanne anatoroka, anakwenda kusikojulikana, huko kusikojulikana ni wapi ambako hawezi kupatikana. Ninafikiri kuna umuhimu wa sheria hii kubadilishwa ili hawa watu ambao wanaowabaka watoto wetu, ambao wanafanya ukatili kwa jamii wasiwe na dhamana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inasikitisha kule Shinyanga mwaka huu mapema mtoto wa mwaka mmoja na miezi 11 alifanyiwa ukatili wa kingono na baba yake wa kambo. Mtoto akaharibika vibaya, Shinyanga Government pale ikashindwa kumtibu ikampeleka Bugando. Lakini huyu mtu aliyefanya unyama huu bado ana haki ya kupata dhamana, kweli akipata dhamana akakaa nje anajua kabisa kwamba ninathibitika nilifanya huu ukatili atabaki, si atakimbia. Vitendo vimeongezeka na ndiyo maana tunajenga jamii ambayo inakuwa ina ukatili, ukiangalia wale watoto wako mitaani Dar es Salaam au hapa Dodoma, wanavuta unga, wanavuta gundi ni kwa sababu ya malezi na ukatili ambao yumkini wamefanyiwa kule nyumbani.

Mheshimiwa Spika, tunatakiwa tuziangalie sheria zetu vizuri, kuangalia ni kwa nini wanapata hiyo favor ndiyo ni haki na ninajua wanasheria sasa hivi wanaoshughulika na haki za binaadam wanajitahidi sana kuhakikisha kwamba inakuja sheria ya makosa yote kuwa na dhamana, lakini kwa kosa la ukatili wa kijinsia kwa watoto na wanaume na wanawake halikubaliki hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa pia nizungumzie kidogo kuhusu suala zima la mikopo ya wanawake, vijana pamoja walemavu. Kwa kweli tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuhamasisha na kuendelea kuhakikisha kwamba fedha kwa ajili ya mikopo ya wanawake, fedha kwa ajili ya mikopo ya vijana, lakini na watu wenye makundi maalum - walemavu wanapata. Niwapongeze sana, sana Wakurugenzi wa Mkoa wa Shinyanga, sisi Shinyanga katika 10 percent ya mikopo hii ambayo wanapewa watu wenye makundi maalum nikiwa na maana ya wanawake, vijana pamoja na watu wenye ulemavu jumla ya shilingi bilioni 18 zimeweza kutolewa katika Mkoa wetu wa Shinyanga hadi kufikia Februari, 2022.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli nawapongeza sana Wakurugenzi pamoja na Waheshimiwa Madiwani kuhakikisha kwamba wanasimamia hizi fedha, ili wanawake waweze kunufaika ni zaidi ya asilimia 91 ya mapato ya ndani kwa kweli ni kazi na ni hatua kubwa sana. Lakini nimpongeze Rais pia kwa kuwajali Wamachinga amewaweka katika group la makundi maalum, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais na tunasikia sijui ilikuwa tarehe ngapi pale, aliweza kusema kwamba atawapa shilingi milioni 10 wamachinga Tanzania nzima kila Mkoa. Kwa kweli hili ni suala la kumpongeza ni jinsi gani ambavyo anawathamini wananchi wake, ni jinsi gani ambavyo anataka kila mtu ajikomboe kiuchumi kwa kweli tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ningependa kuishauri Wizara ya Maendeleo ya Jamii, hii mikopo pamoja na kwamba inatolewa na haya makundi, lakini kule vijijini sina hakika kama hii mikopo kule vijijini inawafikia walengwa wengi. Mikopo mingi hii inatoka kwenye vile vikundi vya mjini ambavyo watu tayari wanauelewa wa nini wanafanya au tayari wameshaanza biashara zao. Ningeomba mjielekeze katika sehemu ambazo ziko pembezoni kule wanawake wana uhitaji, wanawake wanataka kufanya biashara lakini hawajui waanze kufanyaje hiyo biashara.

Mheshimiwa Spika, tungeomba Wizara kupitia Maafisa Maendeleo ya Jamii ambao wako kule pembezoni waweze kuwafikia wanawake wengi, waweze kuwafikia vijana wengi, waweze kuwafikia watu wenye ulemavu ili basi waweze kujikimu na wao waweze kufanya biashara. Lakini ningeomba hili suala la kujenga vituo vya wamachinga ninaomba Serikali ilichukue kwa uzito mkubwa. Tumeona baadhi ya mikoa mfano hapa Dodoma kuna sehemu ambapo inajengwa hilo soko la wamachinga kwa kweli ni soko zuri. Basi hata mikoa mingine iweze kuiga huo mfano, ihakikishe kwamba wamachinga wanatengewa sehemu nzuri, wanaweza kufanya biashara zao bila kubugudhiwa, wanaweza kuendelea kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kunipa hii nafasi ninaomba Wizara hii iwajali pia wale watu ambao ni wanasaikolojia. Tunajua watu wakishafanyiwa ukatili wa kijinsia, wakishafanyiwa ukatili wa kiuchumi, wakifanyiwa ukatili wa aina yoyote ile kisaikolojia wanakuwa hawako vizuri. Kuna hawa watu ambao wamesoma wako barabarani, hawajapata ajira…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, wanasaikolojia tunaomba waajiriwe ili kupunguza tatizo. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kupata fursa ya kusimama kwenye Bunge lako Tukufu kuchangia Wizara ya Nishati. Ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa letu. Tulikumbwa na tatizo kubwa sana la mfumuko wa bei ya mafuta lakini Mheshimiwa Rais kwa jinsi anavyotuthamini Watanzania aliweza kutoa ruzuku ya Bilioni Mia Moja, kwa kweli tunampongeza sana kwa kazi kubwa ambayo anaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwashukuru Wizara ya Nishati Mheshimiwa Kaka yangu Makamba, Watendaji wote na Wasaidizi wako wote kwa kweli mnafanya kazi kubwa sana. Tunajua dunia nzima ina changamoto nyingi na imepelekea mafuta kupanda bei, hili ni janga la dunia siyo janga la Tanzania peke yake. Baada ya Mheshimiwa Rais kutoa fedha kama ruzuku Shilingi Bilioni 100 leo Dodoma nimeenda kununua mafuta angalau yameweza kushuka bei kidogo kama Shilingi 120 hivi, kwa kweli ni juhudi kubwa ambayo inafanywa na Serikali yetu tunajua katika kila mafanikio changamoto hazikosekani tuwaombe sasa kwa bajeti hii ambayo iko mbele yetu ile mipango ambayo mmepanga, nimeona katika jarida hili ambalo mmetupatia mmeweka vipaumbele, ukivisoma hivi vipaumbele unapata matumaini kabisa kwamba Wizara hii inakwenda kufanyakazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijielekeza tu kwenye kipaumbele Namba Mbili cha bajeti hii ambacho kinasema kutekeleza miradi ya nishati vijijini pamoja na kuanzisha utaratibu wa kupeleka umeme katika vitongoji ndani ya nchi. Kwa kweli, suala la umeme hasa huu umeme wa REA vijijini imekuwa ni changamoto kubwa sana. Unakuta kuna Kata ambazo ziko kwenye Manispaa mfano kule Shinyanga, kuna Kata ambayo iko karibu kabisa na grid ya Taifa, pale Ibadakuli ambapo umeme uko pale grid ya Taifa iko pal,e lakini vijiji na vitongoji vya pembeni havina umeme. Hili suala kwa kweli linaumiza sana wananchi wakati mwingine anakuuliza swali unashangaa, anakwambia grid ya Taifa hii hapa ambayo inasambaza umeme kwenda Mwanza, ambayo inapeleka umeme Kahama, ambayo inapeleka umeme Mikoa mingine sisi hapa tunaotoka katika kata ya Ibadakuli hakuna umeme! Kwa kweli huwa inaumiza sana kuona kwamba wananchi wanapata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu kubwa nyingine ni nini? Ni kwa sababu wale wako ndani ya Manispaa wanahesabika kama wako Mjini lakini kiukweli ni kwamba wako kijijini. Vijiji vile ambavyo viko ndani ya Manispaa ningeomba huo utaratibu wa Peri-urban ambao tunausikia mnausema kila wakati lakini utekelezaji wake bado unasuasua. Tunaomba vijiji vyote ambavyo viko ndani ya Halmashauri za Miji au Halmashauri za Manispaa ziweze kupatiwa umeme ili hawa wananchi na wenyewe waweze kufaidika na suala zima la kukuza uchumi. Kwa sababu tunajua umeme ndiyo chanzo kikubwa cha kuhakikisha kwamba vijana wetu wanajiajiri, wengi wamefungua viwanda vidogo vidogo kwa ajili ya kutengeneza mageti, wengine wanachomelea magari, wengine wanatengeneza majiko bila kuwa na nishati ya uhakika ya umeme hawawezi kufanya kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho nataka kukizungumzia ni suala zima la kukatika umeme. Kwa kweli inasikitisha, Wizara mnatufanya tunapata hasara, kwa sababu kama una kiwanda na una shift unalipa wafanyakazi, unategemea wafanyakazi wengine waingie Saa 12 mpaka saa Nane, wengine waingie Saa Nane mpaka usiku, wengine waingie usiku Saa Nne mpaka asubuhi, umeme unapokatika ina maana uzalishaji unadorora, lakini mwenye kiwanda hataacha kuwalipa wale wafanyakazi, matokeo yake nishati inazorota umeme unakatika wanaamua kuwapumzisha vijana ili kubana matumizi. Wenye viwanda wakishabana matumizi tayari wale vijana wanarudi mtaani wanakuwa hawana ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka tujue Mheshimiwa Waziri unapokuja kuhitimisha, tunataka tujue utaratibu wa kudumu mpango mkakati wa kudumu ambao utawezesha huu umeme ukawa stable, kwanza mnatutia hasara unawasha TV, umewasha friji baada ya muda umeme umekatika unarudi unakatika unaweza ukakatika hata mara nane kwa siku, kwa kweli hii haikubaliki ninaomba kabisa Wizara ya Nishati ije na majibu mazuri na mpango mkakati mzuri, umeme wa uhakika mwanzoni tulikuwa tunajua labda wakati mwingine maji sijui katika Bwawa la Mtera yamepungua, mara sijui vitu gani! tunataka mtuambie gesi asili inatusaidiaje kuhakikisha umeme unakuwa stable, mabwawa yanatusaidiaje kuhakikisha umeme unakuwa stable, hizi grid zetu za Taifa zinatusaidiaje kuhakikisha kwamba umeme unakuwa stable? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi wameyafanya katika hii Wizara, kwa kweli hata maneno mengi ya kuongea ninakosa kwa sababu hapa wametu-pre-empty wametupa mpango mzuri, wametupa vipaumbele, wametupa way forward, sasa tunaomba haya mliyoyaandika yatekelezeke, mwaka kesho tukiwa hai kipindi cha bajeti hii ya Wizara ya Nishati, hii itakuwa reference na mkishindwa kuitekeleza hii itabidi tuwaulize tushikiane Shilingi hapa, tuminyane tushikane mashati ili kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wananufaika na nishati ambayo Mwenyezi Mungu ametujaalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ninahitaji kusikia majibu ya uhakika, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Wakala wa Kimataifa wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (International Renewable Energy Agency - IRENA) na Azimio la Bunge kuhusu mapendekezo ya kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika wa Mwaka 2019 (Treaty for the Establishment of the African Medicine Agency - AMA)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kutoa mchango wangu katika mkataba huu wa kuanzishwa kwa Taasisi ya Dawa ya Afrika ya mwaka 2019. Ni ukweli usiopingika kwamba sisi kama nchi tumechelewa. Kati ya nchi hamsini na tano zilizokaa mwaka 2019 kupitisha azimio hili la kuwa na Taasisi hii sisi tumechelewa sana. Leo ndiyo Serikali yetu imeleta Bungeni ili tuweze kujadili na kuridhia mkataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi naomba niunge mkono hoja, na niwashauri na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba turidhie mkataba huu kwa sababu una manufaa kwa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona kwamba Rwanda imepata nafasi au fursa ya kuweza kujenga Makao Makuu ya Taasisi hii. Labda na sisi Tanzania tungeridhia miaka sita iliyopita tangu mkataba huu wamekaa mezani na kusaini na kuridhia kwamba waanzishe Taasisi hii inawezekana kabisa sisi nchi yetu ingekuwa miongoni mwa nchi ambayo kungekuwa na hii Taasisi. Kwa sababu tuna Mamlaka ya Dawa na Tiba ambayo ni bora sana katika Bara la Afrika kwa sababu inakidhi iko katika kiwango cha tatu cha umahiri, na WHO imepitisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi sitakuwa na mambo mengi ya kuzungumza katika mkataba huu; ni mkataba ambao unatija ni mkataba ambao utahimarisha na utadhibiti na kufuatilia masuala yote ya umahiri ya ufanisi wa dawa zote ambazo zitakuwa zinatumika katika bara letu la Afrika hususani Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na dawa nyingi ambazo zinatengenezwa. Nyingine zinatengenezwa na sisi Watanzania kienyeji na zinaingia Tanzania, zinatumika kwa wananchi wetu. Lakini tukishakuwa na taasisi ambayo inadhibiti na kusimamia popote zitakapotoka na popote zitakapokwenda zitakuwa zimehakikiwa, kudhibitiwa, kuwa na ubora halisi na hazitaleta madhara kwa wananchi wetu. Hata kama kutakuwa na madhara basi taasisi hii itakuwa na uwezo wa kudhibiti yale madhara ambayo yatatokana na hizo dawa ambazo wananchi watakuwa wanazitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi niombe kwa mara nyingine, kwa mikataba mingine ambayo ina manufaa kwa Taifa letu. Serikali ijitahidi kuwezesha, kusukuma hili suala ili mikataba kama hii ambayo inajenga na yenye manufaa kwa Watanzania na kwa nchi, inapokuwa imetolewa wailete mapema, waishughulikie, waichakate na ije kwa wakati. Miaka sita toka 2019 mpaka leo ndipo Mkataba unaingia Bungeni binafsi naona kwamba tumechelewa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Rais ambaye ndiye Amir Jeshi Mkuu anaendesha nchi hii kwa sasa hivi. Tangu mwaka 2021 mpaka leo ni kama mwaka mmoja au miaka miwili mkataba umeweza kufika Bungeni; lakini tangu 2019 mkataba uko kwenye mchakato hatujaridhia. Hivyo basi niwashawishi Wabunge wenzangu kwamba mkataba huu kuundwa wa taasisi hii tuweze kuridhia ili na sisi tuwe miongoni mwa nchi hamsini na tano za Afrika ambazo tumeridhia na tutanufaika na mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja, ninakushukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote wa Mwaka 2022
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa kuweza kuchangia katika Muswada muhimu sana wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ya mwaka 2022. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mama Samia kwa kazi kubwa anazozifanya kwa kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ufasaha na kwa umakini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bima kwa wote ni ahadi ya Chama cha Mapinduzi katika Ibara yake ya 83E naomba kunukuu; “Kuhimarisha Mfumo wa Bima ya Afya Nchini ikiwemo Mfuko wa Bima ya Afya NHIF na CHF ili kufikia lengo la Serikali na kuwa na Bima ya Afya kwa Wote,” mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Suala la Bima ya Afya kwa wote ni suala ambalo sisi kama Watanzania tumelisubiri kwa muda mrefu sana. kwa sababu kwanza ni takwa la Kikanda na takwa la Kimataifa lakini pia ni haki ya msingi ya kila Mtanzania kupata Bima ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na sababu mbalimbali ambazo zilipelekea Muswada huu usisomwe mara ya pili, ninaishukuru sana Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha, kuhakikisha kwamba zile changamoto ambazo kama Wabunge tuliziona na tukawa na mashaka, tukajadiliana kwa kina, tukafikia muafaka kwamba Wizara ya Afya ikayapitie yale ambayo tulikuwa tunaona kwamba ni kikwazo yalikuwa hayatubariki. Niwashukuru sana Wizara ya Afya kwa kuwa wasikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo yote ambayo Wabunge walikuwa na wasi wasi kwa sababu sisi Wabunge ndiyo wawakilishi wa Wananchi. Tulikuwa tunatazama kule nje itakuwaje? lakini Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha imekwenda kutekeleza yale ambayo sisi kama wawakilishi wa wananchi tulikuwa tunaamani sana yawepo kwa kweli nawapongeza sana na hii ni juhudi ya Mheshimiwa Rais. Kwa sababu ana dhamira safi ya kuhakikisha kwamba Watanzania wote, Wananchi wake wote wanapata huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiyopingika ukienda kwenye Wilaya, ukienda kwenye Mikoa, ukienda kwenye zahati, zahanati zimejengwa, Vituo vya Afya vimejengwa, hospitali kila halmashauri inayo, zipo ambazo zimekamilika, zipo ambazo zinaendelea kujengwa. Lakini haitoshi bado kuna vifaa ambavyo Serikali ya Mama Samia imevitoa angalia digital x-ray karibia 199, angalia CT scan 32 karibia kila Mkoa una CT scan lakini mashine za MRI na zenyewe zipo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nikijiuliza sana kwamba vitu vyote hivi miundombinu ambayo imetengenezwa. Mwanzoni tulikuwa tuna wasi wasi na idadi ya Watumishi lakini mpaka sasa hivi tunaona kwamba ni takribani asilimia 50.4 ya Watumishi, upungufu uliyokuwepo umeanza kutoweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikawa najiuliza vifaa vyote hivi ambavyo vipo kwenye Hospitali za Wilaya, zipo kwenye zahanati, zipo kwenye Hospitali za Rufaa ni gharama kiasi gani? Je, ni Wananchi wangapi wanaweza wakaweza kupata huduma kwa kutoa fedha zao mikononi? Nikawa najua kabisa kwamba hapa Wananchi wengi wanakwenda kupata matatizo.kwa sababu ni wangapi ambao wanauwezo? tumeona katika Taarifa ya Mheshimiwa Waziri, asilimia 85 ya Watanzania wana kikwazo cha fedha kwenda kupata matibabu katika Vituo vya Afya, katika Zahati, katika Hospitali za Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia maoni ya Wabunge ushauri uliyotolewa na Kamati, Wizara ya Afya ikakaa chini na Wizara ya Fedha ikatoa vyanzo vya uhakika kuhakikisha kwamba Wananchi ambao hawana uwezo wa kuchangia Huduma za Afya kuna Mfuko maalum ambapo Serikali itatoa fedha, itatenga fedha kwa ajili ya Wananchi wote kuweza kupata huduma kwa kujiunga na Mfuko wa Bima ya Afya kwa watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi binafsi pamoja na Kamati ya Afya na Masuala ya Ukimwi tumeridhishwa na Mpango wa Serikali yetu wa bima kwa watu wote kila Mtanzania aweze kupata huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nitoe angalizo kumekuwa na Bima ya Afya (NHIF). Tumeona mapungufu ambayo yalikuwa yakijitokeza na watu waliokuwa wanatibiwa na Bima ya Afya ya Taifa hawakuwa wengi kama ambavyo tunakwenda kuwapata wengi sasa Watanzania wote wataingia kwenye Mfumo wa Bima ya Afya. Yale matatizo ambayo tulikuwa tunayaona ukosefu wa madawa, ukosefu wa Watumishi ambao wana weledi;

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wizara ya Tamisemi kuhakikisha kwamba Wananchi wote watakao jiunga katika Mfumo wa Bima ya Afya kwa watu wote wanapokwenda kwenye Zahanati, wanapokwenda kwenye Kituo cha Afya, wanapokwenda kwenye Hospitali wapate huduma inayoridhisha, wapate huduma ambayo ni rafiki kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kuwashawishi wananchi wote itakapofika wizara itaanza kutekeleza hii azima yake ambayo Chama cha Mapinduzi na Serikali yake inahitaji kuwahudumia wananchi tuwape ushirikiano. Lakini ushirikiano hauwezi ukatolewa kama hatutawaelimisha wananchi wetu, tutoe elimu ya kutosha, tuhamasishe na sisi Wabunge ni Mabalozi ikawe agenda yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokwenda kwenye Mikutano yetu ya hadhara tuhakikishe kwamba inakuwa ni moja ya agenda ili Wananchi wetu waweze kujua manufaa ya Mfuko wa Bima ya Afya kwa watu wote iwe rahisi kwa wananchi wetu kujiunga na Mfumo wa Bima ya Afya kwa watu wote ili waweze kupata huduma ambazo zinastahili kuweza kuwahudumia katika matatizo ambayo wanakwenda kuyapata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sitakuwa na mengi ya kusema; mambo yaliyofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi jamani mwenye macho haambiwi tazama, mwenye masikio haambiwi sikia. Tunasikia kila kunapokucha na leo limekuja hili la Bima ya Afya kwa watu wote haijawahi kutokea, tumekuwa tukisuasua, tumekuwa tukijivuta lakini sasa ubwabwa tumeishatengewa, kazi yetu sisi ni kunawa mikono na kula na kuhakikisha kwamba Wananchi wote wanapata huduma ya bima kwa watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono hoja na ninaomba Wabunge wenzangu tuunge mkono hoja. Kwa sababu zile message za kuambiwa naomba fedha ya matibabu, naomba limefanyaje zitapungua kwa sababu kila Mtanzania atakuwa na access ya matibabu bila kikwazo chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)