Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Boniphace Nyangindu Butondo (12 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. BONIFACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Kwa mara ya kwanza nasimama katika Bunge lako Tukufu, naomba nimpongeze Mheshimiwa Spika na wewe Naibu Spika kwa kuchaguliwa kuwa viongozi wetu katika Bunge hili Tukufu. Pia nitumie fursa hii kukishukuru Chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa kuniteua na kupeperusha bendera ya Chama changu Cha Mapinduzi na hatimaye kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Kishapu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwashukuru pia wananchi wa Jimbo la Kishapu kwa namna ambavyo wamenipa kura nyingi za kishindo kwa asilimia 87.4. Vile vile niwashukuru sana Wanakishapu kwa ujumla, lakini niishukuru familia yangu, kwa namna ya pekee nimshukuru mke wangu, lakini niishukuru na familia yangu kwa ujumla kwa namna ambavyo wamenipa ushirikiano kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapata kura za ushindi na hatimaye kufika katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mchango katika Mpango huu wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka mmoja na miaka mitano. Kwanza nianze kwa kuishukuru sana Serikali yangu kwa jitihada kubwa ambayo imekuwa ikifanya. Sote tuna macho ya kawaida na hatuna macho yenye miwani ya mbao, kwa sababu yako mambo mengi ambayo dhahiri na wazi yamekuwa yakionekana ni mafanikio makubwa kwa Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sekta ya Elimu; sote tunafahamu elimu ya sekondari kwamba sasa hivi tuna sekondari katika kila kata na baadhi ya kata zingine tumeanza kuongeza sekondari. Pia shule zetu za msingi zimeboreshwa, ukilinganisha na hali halisi ya kipindi cha nyuma. Yapo mambo mengi vile vile kama vile ujenzi wa Standard Gauge, ambao sasa hivi unaendelea kwa kasi kubwa; uboreshaji wa huduma ya Shirika la Ndege. Shirika hili lilikuwa limekufa na sasa hivi maendeleo ni makubwa, sote tunanufaika na huduma hii ya usafiri wa anga; kuna mradi huu mkubwa wa ufuaji wa umeme wa Mwalimu Nyerere, ni hatua kubwa ambayo Serikali yetu imewekeza na kufanya mradi huu unakwenda vizuri; na suala zima la uanzishwaji wa viwanda vikubwa, viwanda vya kati na viwanda vidogo. Hii ni hatua kubwa ambayo ni dalili tosha kwamba hatua ya kimaendeleo katika nchi yetu tunakwenda vizuri..

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi kwa sababu sisi siyo wananchi isipokuwa ni taasisi za kifedha za kimataifa ndizo zilizofikia hatua ya kuiona Tanzania inastahili kuingia katika uchumi wa kati. Kwa hiyo tupo assessed kwa utaratibu wa kitaaluma kabisa kabisa na ndiyo maana tumefika mahali tumeingia katika uchumi wa kati.

Kwa hiyo ni jukumu letu Watanzania kuweka mbele uzalendo ili mradi tuhakikishe uchumi wa kati lakini katika kipato cha juu, sisi wenyewe Watanzania kama wazalendo tuhakikishe kwamba tunapambana na tunakuwa wamoja kuhakikisha kwamba maendeleo ya uchumi wetu yanapaa inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie tu mafanikio haya yanaonekana kwenye Jimbo langu la Kishapu, huwezi ukaamini kwa miaka nane ya nyuma na huko nyuma zaidi coverage ya maji ilikuwa chini ya 20%, lakini leo tunavyozungumza nina Mradi mkubwa wa Maji ya Ziwa Victoria ambao kwasasa hivi coverage ya maji pale iko kwenye asilimia 50. Miradi inayotekelezwa baada ya miezi kama minane nina uhakika nitaweza kufikia coverage ya 70%. Hii ni hatua kubwa sana,

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara zinazojengwa kwa kasi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza haya nataka niseme kwamba, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu ameendelea kutujalia afya. Pia naomba niendelee kukushukuru wewe sana kwa sababu nimepata nafasi ya kuchangia jioni hii katika bajeti hii muhimu ya Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu hasa nitajielekeza katika eneo la TARURA pamoja na elimu na kidogo nitagusia upande wa afya. Kwanza, naungana mkono kabisa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba ipo haja ya kuitizama TARURA kwa macho mawili na hasa katika eneo zima hili la kuongeza hii percentage ya kiasi ambacho TARURA wamekuwa wakipewa fedha kwa ajili ya kushughulikia barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo kubwa lenye mtandao mkubwa unaohitaji kutengenezwa ama kulipa kipaumbele ni eneo la barabara zilizopo vijijini. Eneo la Kishapu tuna jumla ya kilometa 1,030 ambazo zinahitaji kutengenezwa lakini zikiwa katika mazingira magumu kweli kweli. Yapo maeneo mengine yapo katika mbuga hasa lakini vile ni vijiji na kuna maeneo ya kiutawala ya kata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa vyovyote vile huduma ya barabara ni ya msingi sana kwa sababu bila huduma ya barabara huduma hizi zingine; kwa mfano huduma ya afya wananchi hawawezi wakayafikia maeneo kwa ajili ya kwenda kupata huduma iwe katika health centre au dispensaries lakini hata katika sekta ya elimu kuna wakati watoto wanashindwa kufika maeneo ya shule kutokana na matatizo ya maji na hasa panapokuwepo na matatizo ya vivuko kadhaa kuharibika Zaidi, kwa hiyo, lipo tatizo kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia usafirishaji wa mazao kila mmoja hapa anafahamu Mkoa wa Shinyanga ni Mkoa ambao unalima sana pamba. Tunapozungumza zao la pamba ni Wilaya ya Kishapu ndiyo inayoongoza kwa kulima pamba. Tafsiri yake Wilaya ya Kishapu ni moja kati ya wilaya na inawezekana ikawa ya kwanza ama ya pili nchini kwa uzalishaji wa pamba. Sifa ya zao la pamba katika kuchangia uchumi wa nchi hii unaweza ukawaona hawa wana Kishapu ndiyo wanaongoza kwa adha ya barabara, hapa hakuna haki kabisa. Nataka niishauri sana Serikali na hasa Wizara yetu ione umuhimu wa Wilaya ya Kishapu kuhakikisha kwamba barababara zinatengenezwa na inaongezewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niyataje baadhi ya maeneo ambayo yana hali mbaya kabisa, zikianza tu kunyesha mvua safari za kuelekea Kata za Itilima, Kiloleli, Mwaweja na Mwamalasa inakuwa ni shida, hizi ni kata ambazo hazipitiki kabisa. Hili ni tatizo ambalo kwa kweli tusipoliangalia tunaweza tukawakatisha tamaa sana wananchi. Zipo Kata za Uchunga, Mwataga na Somagegi, hizi ni kata ambazo na zenyewe zinakuwa kisiwani pale mvua zinapoanza kunyesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna haja ya Serikali kulitazama eneo hili na kuona haja ya kupeleka fedha za kutosha. Wenzangu wameshauri sana katika masuala ya simu, hili jambo tunaweza tukaliangalia na Serikali ifike mahala iwe serious, tuwahurumie wananchi. Bunge limekuwa likitoa mawazo hata katika eneo la mafuta, kwa nini tusifike mahali tukajifunga mkanda lakini lengo tuwafungulie njia wananchi? Nasema hivi kwa sababu Watanzania kwa ujumla wanahangaika na masuala ya barabara. Kwa hiyo, mimi naamini kwa sababu Serikali ya CCM ni sikivu kupitia mMwaziri wetu na hususani Mheshimiwa Ummy Mwalimu pamoja na wasaidizi wake ndugu yangu Mheshimiwa Silinde na Mheshimiwa Dkt. Dugange mfanye hili jambo ili mradi tuwapunguzie adha wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepata habari kwamba kuna kama shilingi bilioni 100 zimeongezeka kidogo na wengine wameshaanza kupata taarifa, zimeshaanza kutumwatumwa kule, mimi naomba Kishapu tuikumbuke. Tuikumbuke Kishapu kwa jicho la huruma kwa sababu wananchi hawa wanateseka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nataka nizungumzie ahadi za viongozi wetu wakuu. Kipindi cha Uchaguzi aliyekuwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alifika Kishapu na bahati nzuri aliweza kuahidi kilometa nne. Ahadi hii alikuja kusisitiza kwa sababu alishaiahidi awamu ile ya kwanza, maana yake miaka mitano barabara hiyo ilikuwa haijatekelezwa lakini imeanza kutekelezwa kwa mwaka fedha uliopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi kilometa nne tumepata jumla ya shilingi milioni kama 114, shilingi milioni karibu 380 zilikuwa hazijafika. Naomba sana fedha hizi ziweze kufika na kusaidia wananchi hawa ili mradi Mji wa Kishapu na wenyewe uweze kufanana. Kwa sasa hivi kazi iliyopo kwenye ile kilometa moja kuna asilimia kama 94, lakini nachoomba Wizara iweke msukumo na kuhakikisha fedha zile zinafika Kishapu na kuhakikisha kwamba mradi huo tunaukamilisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna upungufu wa walimu 1,611 katika shule za msingi, hapa kuna tatizo kubwa sana. Kwenye nyumba za walimu na penyewe pana shida kubwa. Kuna tatizo kubwa sana upande wa madarasa, wananchi wamejitahidi sana kutoa nguvu zao kuhakikisha kwamba wanasukuma mbele na kutoa mchango upande wa madarasa. Hata hivyo, kuna haja Serikali kuweka mpango maalum kuhakikisha kwamba ina-support nguvu za wananchi, yako magofu mengi ambayo yanahitaji support na hii ni katika shule za msingi na sekondari. Naomba sana Wizara hii iweze kutazama maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna Kata mpya za Shagihilu, Mwaweja, Bupigi, Mwasubi, Mwadui, Luhumbo na Mwamala tumeshaanzisha sekondari mpya na bahati nzuri Serikali imekuja na mpango wa kuhakikisha inapeleka fedha kwa ajili ya sekondari hizi. Naomba sana Wilaya ya Kishapu ipewe kipaumbele na wananchi hawa tusiwakatishe tamaa tuhakikishe tunawapelekea fedha kwa ajili ya kuhakikisha maeneo haya yanafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni upande wa Waheshimiwa Madiwani na nataka nizungumzie maslahi yao. Nimekuwa Diwani kwa zaidi ya miaka 20 na nimekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri kwa zaidi miaka 10. Nataka nizungumze Madiwani wana shida kubwa sana na kusema ukweli hawa Madiwani ndiyo wanaosimamia shughuli za maendeleo, ndiyo wanahamasisha shughuli za maendeleo. Hawa Madiwani ndiyo wanaotoka jasho kwa ajili yetu sisi Wabunge ili mradi tupate ushindi pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kuna kila sababu Mheshimiwa Ummy, Mheshimiwa Silinde, Mheshimiwa Dkt. Dugange oneni huruma kwa hawa viongozi wenzetu waongezeeni posho, laki tatu na siyo hela. Jamani tuangalieni majukumu waliyonayo na wananchi wanaowahudumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine hawa watu posho zao za vikao ni matatizo makubwa sana, ipo shida kubwa. Pengine na mimi nilikuwa naungana mkono tuhamishe posho hizi za madaraka ziwe zinalipwa na Serikali Kuu tubaki na hizi posho za vikao kwa sababu mzigo kwa baadhi ya Halmashauri unakuwa ni mkubwa na Halmashauri zinashindwa kulipa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi iliniweze kuchangia katika Wizara hii muhimu inayoshughulikia masuala ya miundombinu na hasa barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, naomba niwapongeze Mawaziri; kwa maana ya Waziri pamoja na Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote katika Wizara hii. Kazi wanayoifanya ni kubwa lakini kusema kweli changamoto bado ni nyingi. Tunahitaji kuongeza nguvu zaidi kuhakikisha kwamba barabara zinapitika kwa sababu msingi wa uchumi wetu unahitaji sana kuimairisha miundombinu na hasa barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kama Tanzania hii tumeamua kusimama na kuamua Tanzania yetu iwe ni Tanzania ya viwanda. Viwanda hivi bila kuwa na barabara nzuri, uhakika wa viwanda vyetu kuzalisha na kuwa na ufanisi bado utaendelea kuwa ni hadithi. Pia tunafahamu kwamba bila barabara nchi yetu inategemea kilimo na kilimo ndiyo uti wa mgongo, wakulima wetu wataendelea kupata shida ya kusafirisha mazao na hivyo na wao wataendelea kutokupata tija katika shughuli yao ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla shughuli zote za kijamii, ziwe huduma za afya na maeneo mengine kama hatujajipanga vizuri katika eneo hili la miundombinu bado Tanzania tutaendelea kusuakusua kwenda mbele katika shughuli za kimaendeleo. Kwa hiyo eneo hili ni eneo muhimu sana, hivyo Serikali nchi nzima bila kujali eneo fulani ama maeneo ya mijini, iwe vijijini ni lazima igawanye sawa hii keki kama Waheshimiwa Wabunge wenzangu ambavyo wamechangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nizungumzie katika bajeti ya hii ambayo tunaijadili, kusema ukweli katika eneo langu na hasa Kishapu unaweza ukaona ni kana kwamba hakuna barabara yoyote mpya ambayo imeweza kuwekewa fedha hapa. Kuna barabara ambayo hapa imeainishwa ni Barabara ya Kolandoto yenye urefu wa kilometa 62.4. Barabara hii ya kutoka Kolandoto ambayo inakwenda mpaka Mwanuzi hizi kilometa 62 sote ni mashahidi ni kilometa nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukaona labda ni fedha ambazo zimewekwa kwa ajili ya kushika kifungu ni bilioni mbili, bilioni mbili hizi zinakwenda kutengeneza kilometa ngapi? Ni mambo ambayo unaweza ukashangaa. Barabara hii ni barabara ambayo imekuwepo hata katika Ilani ya mwaka 2015 - 2020, lakini barabara hii haikuweza kutengewa fedha, lakini katika kipindi hiki imetengewa peke yake, jumla ya shilingi bilioni mbili peke yake. Fedha hizi ni kwa ajili ya kufanya nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine wananchi wetu wanaweza kufika mahali wakasema hii ni habari ya utani. Walikuwa wanataka majibu sawasawa katika hatua ile ya majumuisho ya mwisho ya Mheshimiwa Waziri kwamba nini mpango wa Serikali kwa sababu fedha hizi ni fedha za ndani lakini kama pengine kuna mikakati ya kupata fedha za nje nataka nipate majibu sawasawa na vinginevyo naweza nikaona kwamba wananchi wetu wanaendelea kuvunjika imani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais, aliyekuwa Rais wetu Marehemu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alisema kwamba barabara hii ni lazima tuitekeleze na akawakumbusha wananchi tuliweka kwenye mpango katika kipindi kilichopita hatukutekeleza tunawahakikishieni tunakwenda kuitekeleza. Kwa hiyo hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, lakini kwa sababu imo kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi ni lazima tujipange tuhakikishe kwamba barabara hii tunaitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukaona katika barabara nyingine ya Mwigumbi kwenda Maswa, hii ni barabara ya lami ambayo ipo tayari. Kitu ambacho kinasikitisha pengine labda nipate majibu katika, ukiangalia kwenye bajeti hii barabara hii imetengewa bilioni 50.3, sasa bilioni 50.3 hizi sijajua ni kwa ajili ya nini kwa sababu barabara hii ilishakamilika na kuna maeneo ambayo yalikuwa mabovu yalishafanyiwa matengenezo. Kwa nini fedha hizi zisingepelekwa kwenye barabara hii ya kutoka Kolandoto kwenda Mwanuzi kuja Kishapu. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya ni mambo ambayo pengine nataka nijue hizi bilioni 50 ni kwa ajili ya kufanya nini? Kwa sababu tunaendelea kutoa pesa nyingi tunazipeleka kwenye barabara ambayo tayari ilishatengenezwa. Wakati mwingine inaweza ikaleta tafsiri ni mianya rahisi ya kuweza kutumia fedha bila kuwa na maswali mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilitaka nataka nizungumze hili, nipate majibu mazuri kwamba hii bilioni 50 kwa barabara hii ya Mwigumbi kwenda Maswa ni kwa ajili ya nini wakati barabara hii imekamilika. Juzi ilipata matatizo ikafanyiwa maintenance, lakini bado imewekewa fedha nyingi huku barabara ya Kolandoto kwenda Kishapu imewekewa bilioni mbili, nataka tafsiri na maelezo kuhusiana na hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nizungumzie ni suala zima la uwanja wa ndege wa Shinyanga. Mkoa wa Shinyanga tuna shughuli za madini pale Mwadui, lakini tuna wachimbaji wadogo katika Mji wetu wa Maganzo pamoja na eneo lingine, eneo lote linalozunguka maeneo ya Maganzo na wananchi wanazo fedha, lakini Shinyanga tunalima pamba, habari ya fedha kwetu siyo tatizo. Kwa hiyo, habari ya usafiri wa ndege wala hata sisi kwetu siyo habari mpya kwa sababu ni watu ambao tunazo fedha bwana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Uwanja wa Ndege wa Shinyanga imekuwa ni hadithi, hadithi. Kila mwaka kipindi kilichopita ilikuwemo kwenye Ilani, ilikuwemo sijui kwenye bajeti mbalimbali, uwanja wa Shinyanga unaenda kukarabatiwa, kila mwaka ni habari ya hadithi hizi. Jamani katika Wizara hii kuna matatizo gani? Uwanja huu mimi niwaambieni hata kipindi kile ambacho kiwanja hiki kilikuwa kinafanya kazi, kati ya viwanja ambavyo vilikuwa na abiria wengi sana kipindi cha nyuma, kimojawapo ni Kiwanja cha Shinyanga. Sasa sijajua kama wanapiga hesabu ama tunaendelea kujenga viwanja vingine tu bila kuangalia uhalisia na historia ya viwanja vipi ambavyo vinakuwa na wateja wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nipate majibu mazuri kwamba kiwanja hiki kinakwenda kutengenezwa kweli? Unaweza ukaangalia fedha zilizowekwa peke yake ni bilioni 3.6, naziona ni fedha kidogo na kiwanja kile tumekiacha kwa muda mrefu, kilikuwa na uharibu mdogo, lakini viwanja vya aina hii vimeendelea kuharibika, kwa rafiki yangu kule Mhata kule…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Butondo kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa mzungumzaji kwamba ni kweli kabisa nakubaliana naye kwamba Serikali haiangalii viwanja ambavyo vina; mosi, vinakuwa vina historia lakini pia vinaweza kuchangia pato kubwa kwenye uchumi wa Taifa, mfano uwanja wa ndege wa Musoma ambapo anatoka Baba wa Taifa, tuna madini kule, tuna ziwa, tuna Mbuga za Wanyama na vitega uchumi kibao lakini mpaka sasa hivi unasua sua tu, nilikuwa naomba nikupe hiyo taarifa Mheshimiwa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Butondo unapokea taarifa hiyo.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kwa sababu hoja ya Mheshimiwa Matiko ni ya maslahi mapana kabisa ya Taifa letu nimeipokea taarifa yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka nizungumzie kwa Mheshimiwa Mhata, Kiwanja kile cha Masasi ni aibu, ni moja kati ya maeneo ambayo nilitaka nizungumze kwa uwazi. Kiwanja kile kilifikia hatua mbaya, hata kile kipindi tunakwenda kumhifadhi cha mzee wetu, ilifanyika kazi ya kuchoma nyasi zile, ndiyo ile helikopta ikatua pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavisahau viwanja vikongwe na viwanja ambavyo tumekuwa tukisema mwaka kila baada ya mwaka kwamba vitakwenda kukarabatiwa. Hii ndiyo habari ambayo wanazungumza wenzangu, Mheshimiwa Mwenisongole amezungumza kwamba keki hii


ni lazima tuigawanye katika usawa. Kwa hiyo nataka niiombe sana Wizara, tusije tukajenga tafsiri ya kwamba kwa kweli kuna baadhi ya maeneo watu wengine wanapendelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata katika hotuba hii maeneo mengine tusingependa kuyafungua na kuzungumza, baadhi ya maeneo yamepewa fedha tena fedha nyingi, lakini baadhi ya maeneo mengine hatuna fedha, pengine inaweza ikaleta tafsiri nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nataka hili nilizungumze naikumbusha Wizara kwamba iwe makini kuhakikisha kwamba maeneo yote hasa ya msingi yanatazamwa na fedha zinapelekwa kwa ajili ya kusaidia wananchi katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie, ni kuhusiana na daraja. Lipo daraja moja ambalo limejengwa katika Jimbo langu la Kishapu. Daraja la Buzinza, Kishapu - Buzinza na daraja lile linaunganisha pia Wilaya ya Igunga. Daraja hili limejengwa kwa thamani ya shilingi bilioni 2.3, lakini tangu daraja hili litengenezwe leo ni zaidi ya miaka mitatu daraja hili limekamilika, lipo katika Mto Manonga, lakini baada ya kukamilika daraja hili halifanyi kazi kwa sababu nyakati za masika kushoto na kulia yaani unapokuwa unavuka na unapokuwa unavuka upande mwingine mto ule unatakiwa ujengelee sasa barabara. Kivuko cha kutoka huku na kivuko cha kutoka huku, kwa sababu ule ni mto.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni sawa na kwamba Serikali imekwenda kutupia zile fedha halafu barabara hiyo haina maana yoyote. Niombe sana Wilaya ya Igunga na Wilaya ya Kishapu iunganishwe kupitia daraja hili vinginevyo ni sawa na kwamba tumezimwaga zile fedha na hakuna maana yoyote ya kupeleka hizo fedha. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili imegonga.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, ilikuwa ya kwanza.

NAIBU SPIKA: Imeshagonga ya pili, ahsante sana.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia. Kwanza nami naomba nimshukuru sana na nimpongeze sana Mheshimiwa Biteko pamoja na Naibu Waziri wake kwa namna ambavyo wamekuwa wakisimamia vizuri sana sekta hii ya madini na Watanzania wote wanaona mafanikio na sote kwa ujumla tunanufaika kwa kuongeza pato la Taifa kwa asilimia zaidi ya tano kutokana na sekta hii ya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kwanza nataka nizungumzie kuhusiana na suala la Mgodi wa Mwadui. Mgodi wetu wa Mwadui sote tunafahamu kwamba, Serikali ina asilimia 25 na mwekezaji asilimia 75, lakini Mgodi huu tangu tarehe 8/4/2020 umesimamisha uzalishaji, lakini suala hili limetokana na kwanza kulikuwepo na kuporomoka sana kwa bei ya Soko la Dunia la Almasi na sote tunafahamu soko lile la almasi liko Ubelgiji peke yake.

Mheshimiwa Spika, baada ya tatizo hilo, muda ule ule palitokea tatizo la Covid 19 na tangu kipindi kile mgodi wa Mwadui hadi sasa tunavyozungumza; tangu tarehe 8 ya mwezi wa Nne, mpaka sasa mgodi huu haufanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, tunaweza tukajua pale katika eneo lile kuna watumishi zaidi ya 1,200, sasa Serikali inaweza ikaona tu kwamba kuna watumishi wengi sasa ambao wanapata shida na mahangaiko makubwa. Tatizo kubwa hili la kuteremka kwa bei ya almasi, bado ni changamoto hadi sasa, lakini angalau kuna improvement; na juzi waliamua kuanzisha uzalishaji, tatizo linalosumbua pale ni mtaji kwa ajili ya kuhakikisha mgodi ule sasa unaanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, ziko taratibu ambazo wameanzanazo ili mradi waanze ku-run huo mgodi na waanze kuzalisha, lakini tatizo kubwa ni mtaji wa kuanzia kwa sababu, zinatakiwa dola milioni 25 ambazo unaweza ukaona ni karibu shilingi trilioni tatu. Fedha hizi ni fedha nyingi. Kuna wakati wamezungumza na CRDB na NMB. CRDB walionesha mwelekeo wa kutaka kusaidia Mgodi wa Mwadui ili mradi uanze kuzalisha, lakini baadaye walirudi nyuma. Wameanza mazungumzo na NMB, lakini NMB mpaka sasa hivi hawaja-respond sawa sawa.

Mheshimiwa Spika, ombi langu ni Serikali kuweka mkono wake ili mradi waone kwamba mgodi huu unaanza kuzalisha. Faida kubwa ya mgodi huu iko kote kote; kwenye Halmashauri kuna Service Levy ambayo Halmashauri Halmashauri ya Kishapu itaweza kupata, lakini kuna CSR ambayo inaweza ikasaidia mambo mengi sana kusukuma mbele shughuli za maendeleo, lakini na Serikali inapata mapato makubwa kutokana na mgodi huu. Kwa hiyo, naiomba Serikali iweke jitihada za karibu sana, pengine wazungumze na waweke mkono wao ili CRDB ama NMB waweze kutoa fedha na mgodi huu uanze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna tatizo lingine katika mgodi huo. Kulikuwepo na suala zima la almasi ambazo ziliweza kukamatwa zilizokuwa na matatizo, Serikali imeshughulika na baadhi ya watumishi wetu walihusika katika kuhujumu. Tatizo hilo nadhani lilienda Mahakamani likazungumzwa likafikia hatua za mwisho.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naiomba Serikali iweze kutoa maamuzi, ikiwezekana kama sehemu hiyo ingefaa kurudishiwa sehemu ya zile mali Mgodi wa Mwadui waweze kurejeshewa, lakini hatua zile za kisheria kwa watumishi wetu ambao walikiuka ziweze kuchukuliwa, lakini mgodi uweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kuna masuala yale ya VAT kabla ya sheria haijaweza kubadilishwa, Serikali iweze kuangalia. Kwa sababu, kuna VAT ambazo zilipaswa kurejeshwa katika mgodi huo, hizi nazo pamoja na mali zitakazorejeshwa zinaweza zikasaidia mgodi ukaweza kufanya kazi yake…. (Sauti ilikatika)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nataka kuzungumzia suala la migogoro ya mipaka kati ya Nyenze na Ng’wang’holo. Kuna mwekezaji aitwae El-hilal ambaye eneo lile la Mwan’gholo na Nyenze kabla ya miaka miwili huko nyuma wananchi walikuwa wanalitumia kwa kilimo, kuchunga na mambo mengine, lakini juzi wachimbaji wadogo wakaja kuibua madini ya almasi, lakini huyu mwekezaji aliibuka na kusema eneo lile ana hati.

Mheshimiwa Spika, kipindi cha uchaguzi, aliyekuwa Rais wetu mpendwa Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alielekeza jambo hili kwamba anakwenda kulishughulikia kwa sababu alitambua kwamba wananchi ndio waliogundua kule, lakini akaona ukubwa wa eneo hilo na akasema kwamba ipo haja ya wachimbaji wadogo kukatiwa sehemu ya eneo hilo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Boniphace!

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba Serikali iweze kuchukua uamuzi na kuweza kufidia ili mradi…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: …wachimbaji wadogo waweze kupewa eneo hilo, lakini pia Wizara ya Ardhi waweze…

SPIKA: Mheshimiwa Butondo.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: … katika eneo hilo… (Sauti ilikatika) (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Wachimbaji wadogo leo wana watetezi kweli kweli.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara muhimu kabisa ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninaomba na mimi nirudishe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama Samia Suluhu Hassan. Hii ni kwa namna ambavyo Watanzania tumeshahudia fedha nyingi zikiletwa katika majimbo yetu katika sekta mbalimbali na wananchi wamekuwa wakishihudia na kujionea wenyewe jitihada kubwa za maendeleo katika sekta zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie pia nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wake wote, Katibu Mkuu na Watendaji wengine wote katika Wizara hii ya TAMISEMI kwa namna ambavyo wamejipanga kuhakikisha wanasimamia wizara hii vizuri; na sisi wananchi wa Kishapu tunawapongeza kwa namna ambavyo wamekuwa pamoja kabisa kuhakikisha kwamba mambo ya maendeleo yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza Mkuu wangu wa Mkoa Mheshimiwa Mdeme. Mkuu wangu huyu ni Mkuu wa Mkoa wa aina ya pekee kwa sababu ana ushirikiano wa karibu na sisi Wabunge na halmashauri zetu zote katika Mkoa wa Shinyanga. Nitumie nafasi hii pia kumshukuru Mkuu wa wangu wa Wilaya Mheshimiwa Mkude, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri Bwana Emmanuel Johnson, pia nimshukuru Mwenyekiti wa Halmashauri yangu ya Kishapu na Waheshimiwa Madiwani kwa namna ambavyo tunashirikiana kwa pamoja kupeleka mbele maendeleo katika wilaya yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nikuhakikishie kwamba nimepokea zaidi ya bilioni 11 kwa mwaka wa fedha uliopita lakini mpaka sasa nimeshapokea tena bilioni nane ambazo bilioni hizi zimekwenda kutekeleza shughuli mbalimbali za kimaendeleo kwenye jimbo langu ikiwemo sekta ya barabara, maji, elimu, afya na maeneo mengine yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya mambo ambayo nataka niyazungumzie katika eneo la barabara, nimepokea zaidi ya bilioni 2.43. Fedha hizi mpaka sasa ninavyozungumza ipo miradi muhimu kabisa ambayo inatekelezwa. Mradi wa Mwajidalala Bulekela ambapo kuna kunyanyua daraja na kuweka makalavati, barabara ambayo inakwenda kuunganisha Wilaya ya Kishapu na Wilaya ya Igunga. Pia kuna Mangu-Somagedi kuna fedha, tayari sasa hivi fedha zipo na mradi unatekelezwa; na Ngunga pamoja na maeneo ya Munze. Kuna barabara ya Seseko, Busangwa, pia kuna Barabara ya Buganika Kabila. Barabara hizi zote mpaka sasa hivi wakandarasi wako site na shughuli zinakwenda vizuri. Kwa hiyo katika eneo hili la TARURA ninashukuru kwa sababu miradi mingi naamini kwamba itatekelezwa na maeneo haya yote yalikuwa maeneo korofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba TARURA wanafanya kazi nzuri sana na ninaomba tuamine. Meneja wa TARURA wilayani kwangu Kishapu anafanya kazi nzuri na sisi Madiwani tunampa ushirikiano mzuri kazi zinakwenda vizuri. Jitihada zinazotakiwa ni kuwaongezea fedha…

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili barabara nyingi ziweze..

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Butondo.

TAARIFA

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanta sana nataka kumpa taarifa Mheshimiwa anayechangia, ukiifungua barabara inayotoka Kishapu kwenda Igunda utakuwa umeunganisha Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Simiyu, kama ambavyo sera yetu inasema kila mkoa uunganishwe na barabara ya lami kwa maana ya barabara kubwa. Pia itakuwa ni shortcut nyepesi ya kutoka Simiyu Shinyanga kupita Tabora kwenda Mbeya, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Butondo unaipokea hiyo taarifa.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa ya Mheshimiwa, ni taarifa ya muhimu kabisa. Naomba niendelee upande wa sekta ya elimu. Katika sekta ya elimu tuna upungufu mkubwa wa walimu kwanza mahitaji ni 1983 waliopo ni 922 upungufu ni 1,061, ni idadi kubwa sana ya walimu. Sasa kama tunasema kipaumbele chetu katika nchi yetu ni elimu, elimu, elimu, ni lazima jitihada kubwa ifanyike kuhakikisha kwamba tunaongeza walimu ili mradi tatizo hili liweze kuondoka. Vivyo hivyo hata katika sekondari mahitaji ni 482 waliopo ni 403 pungufu ni 79, bado ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu katika ajira hizi zilizotangazwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naomba sana kipaumbele wapewe walimu ambao wamekuwa wakijitolea katika maeneo yetu; na hii tumejionea wenyewe. Tumekuwa tukipata ajira za watumishi kutoka maeneo mbalimbali lakini wanapofika katika maeneo hayo, baada ya muda mfupi wimbi kubwa la watumishi wanaandika barua za kuomba kuhama. Sasa kwa nini Serikali tunatumia resources nyingi kwa ajili ya kuhamisha, kuwaondoa mahali pengine na maeneo mengine yanabaki kuwa na ma-gape makubwa na hasa ambayo yako pembezoni? Naomba sana, hawa walimu wanaojitolea hata katika sekta ya afya pia tuweke kipaumbele na tuwatizame, kwa sababu tayari wakurugenzi, maaifisa elimu wamekuwa wakitoa taarifa huku wizarani, zinazoonyesha walimu wanaojitolea lakini na madaktari wanaojitolea, hawa ndio wapewe kipaumbele katika ajira hizi zitakazokuwa zinatangazwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie mahitaji katika sekta ya afya. Tunahitaji watumishi 664 lakini waliopo ni 274 na upungufu ni 391; unaweza ukaona kwamba ni upungufu mkubwa sana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niishukuru sana Serikali ya Mama Samia kwa namna ambavyo mmeweza kutusaidia katika Hospitali yetu ya Wilaya, kwa mwaka uliopita tulipata bilioni 1.3 Hospitali yetu ya Wilaya, Kalitu tulipata milioni 900, milioni 500 Negezi, milioni 300 Mwangalanga na Shinongela milioni 50. Lakini kwa mwaka huu wa fedha Jakaa tulipata milioni 500, Hospitali yetu ya Wilaya tumepata milioni 50, Wella dispensary tumepata milioni 500 Mwamalasa. Hii miradi mpaka sasa ninavyozungumza inakwenda kwa kasi. Naomba niwapongeze sana Madiwani wangu kwa namna ambavyo wamejipanga kusimamia na kuhakikisha kwmaba miradi hii inakwenda vizuri, na niishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi lingine, ninaomba sana; kuna maboma zaidi ya 32 ambayo yanahitaji kukamilishwa katika sekta ya afya. Kwa hiyo nitoe ombi kwamba katika eneo hili tuone umuhimu wa kupeleka fedha za kutosha kwa ajili ya kukamilisha maboma. Jambo lingine nilitaka nizungumzie upande wa ukaguzi. Tumeshuhudia kwamba taarifa ya CAG kwa sehemu kubwa tumeona upotevu mkubwa wa fedha. Sasa napozungumzia katika halmashauri hatuwezi tukawa na halmashauri imara na zinazosimamia vizuri taratibu, kanuni zile za kifedha na matumizi ya fedha kama hatujawa na wakaguzi wa kutosha katika halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu ina mkaguzi mmoja tu wa ndani. Nataka niulize kata 29 halmashauri penyewe pale Makao Makuu, huyu ni mkaguzi mmoja anawezaje kusimamia shughuli hizi zote katika wilaya ya nzima? Ipo miradi inayotekelezwa katika ngazi ya kata, ipo miradi inayotekelezwa ngazi ya wilaya, majengo mbalimbali, miradi hii inayotokana na mapato ya ndani, fedha za ruzuku na wahisani wengine mbalimbali huyu anajigawa vipi, mkaguzi wa ndani mmoja peke yake? Akiugua homa mwezi mmoja halmashauri ina-paralyze. Hebu tuangalie mama yangu kama kweli una nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba hizi hati chafu, huu upotevu wa fedha hautoki ni lazima tufanye mikakati ya lazima kuhakikisha tunapeleka wakaguzi katika halmashauri zetu. Hili nilitaka niombe sana lifanyiwe kazi ili tuweze kudhibiti haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusiana na suala la Madiwani. Tumezungumza kwa muda mrefu kwamba Waheshimiwa Madiwani walipwe kupitia Serikali, tunaishukuru Serikali kwa uamuzi wake kuamua kulipa fedha hizi moja kwa moja kupitia Serikali Kuu, lakini bado changamoto kubwa ni suala zima la fedha wanazolipwa, ni kiasi kidogo sana. Majukumu wanayoyafanya na kusimamia mabilioni haya hayastahili na kile ambacho wanalipwa kutokana na usimamizi wanaofanya. Hebu tuoneni utaratibu wa kuwasaidia hawa watu, na ni wa muhimu sana. Sisi Wabunge bila wao hatuwezi chochote kile. Ninaomba sana Serikali muwe wasikivu Serikali ya Mama ni sikivu. Ninakuomba Mheshimiwa Kairuki ufanye jitihada zote kuhakikisha kwamba ushawishi huo unatokea na Waheshimiwa Madiwani waweze kuongezewa stahili zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni waraka unaohusiana na Kamati ya Fedha kufanya ukaguzi wa miradi kila baada ya miezi minne, utaratibu huu ni wa ajabu kabisa. Kanuni zinasema kamati za kudumu zitakwenda kila baada ya miezi minne kwenda kukagua miradi iliyotelekezwa katika kipindi hicho…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Butondo.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Nishati, Wizara ambayo Wabunge takribani wote hapa tumekiri wazi kwamba ni Wizara ambayo ni ya muhimu kabisa kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwanza na mimi nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na hata leo napata nafasi ya kuchangia kwa ajili ya mambo muhimu kabisa yahusuyo nishati. Lakini la kwanza nikupongeze wewe kwa uthubutu wako na kuamua kugombea nafasi hii katika Bunge la IPU. Nataka nikuhakikishie sisi Wabunge tutaendelea kukuombea wakati wote ili mradi haya aliyoyazungumza Mheshimiwa Matiko kama mjumbe wako kuhakikisha kwamba na sisi maombi yanaungana pamoja na nyinyi kuhakikisha kwamba unapata ushindi wa kishindo katika uchaguzi huo unaokuja.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee naomba nimpongeze Mheshimiwa January Makamba Waziri katika Wizara hii ya Nishati kwa namna ambavyo amekuwa akifanya kazi nzuri ya kuisimamia Wizara hii; na mabadiliko makubwa katika kipindi chake cha uongozi sisi wenyewe tumekuwa mashuhuda na Watanzania wamekuwa mashuhuda katika mapinduzi makubwa ambayo umekuwa ukipambana wakati wote ili kuhakikisha kwamba azma ya Watanzania na Serikali inaweza kufikiwatena katika kiwango kinachotakiwa.

Mheshimiwa Spika, nimpengeze sana Mheshimiwa Byabato ambaye ni Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji katika Wizara hii. Pia naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Meneja wangu wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga pamoja na Wilaya yangu ya Kishapu kwa namna ambavyo wamekuwa wakisismamia vizuri suala zima la umeme katika Wilaya yangu ya Kishapu na Mkoa mzima wa Shinyanga.

Mheshimiwa Spika, kuna kampuni hii ya Suma JKT ambaye ndiye mkandarasi anayesambaza umeme katika Wilaya yangu ya Kishapu. Naomba nimpongeze kwa sababu kwa kweli kazi inayofanyika ni kubwa na changamoto ilikuwa ni kubwa kwa sababu tulikuwa na idadi kubwa ya vijiji ambavyo havikuwa na umeme kabisa, na sasa tunaona mabadiliko makubwa yanayoendelea katika sekta hii muhimu katika Jimbo langu la Kishapu.

Mheshimiwa Spika, na moja kwa moja naomba niunge mkono hoja kwamba bajeti hii yenye thamani ta trioni tatu iweze kupita kwa asilimia 100 kwa manufaa ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, la kwanza katika mchango wangu naomba Mheshimiwa Waziri nikupongeze sana kwa kusimamia suala zima la Mradi wa Umeme wa Jua ambao tarehe 29 Mei tumeweza kusaini mkataba huu na kuushuhudia sisi Wabunge pamoja na Kamati ya Kudumu ya Nishati ya Bunge kwa namna ambavyo mradi huu unakwenda kuwanufaisha Watanzania.

Mheshimiwa Spika, Mradi huu upo katika jimbo la kwangu la kishapu katika Kata ya Taraga Kijiji cha Ngunga; na tunakwenda kuzalisha megawatt tano na mradi huu ni wa thamani ya zaidi ya bilioni 275. Kwa kweli mradi huu ukishakuwa umekemilika hizi megawatt tano zinaweza kuongezwa katika Grid ya Taifa, na kwa hali hito tunaenda kupunguza pakubwa sana tatizo la umeme hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, ninaomba tu niseme kwamba mradi huu ni mradi mkubwa wa kwanza, na kwa maana hiyo tunatarajia makubwa yatakuwa yanakuja kwa sababu Mkoa wa Dodoma nao unaenda kupata bahati ya mrado huu mkubwa wa Umeme wa Jua. Sasa kwa msingi huo naomba niipongeze sana Serikali inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano kwa jitihada kubwa anazozifanya kuhakikisha kwamba Watanzania tunaondokana na changamoto kubwa ya umeme katika Taifa letu.


Mheshimiwa Spika, lakini jambo kubwa ambalo naliona katika mpango huu wa umeme huu wa jua ambao katika Wilaya ya Kishapu tunaenda kunufaika nao; kwanza tunaenda kupata service levy kwa ajili ya Halmashauri yetu ya Wilaya ya Kishapu ambayo tunakwenda kuongeza mapato ya ndani ya halmashauri yetu kwa sehemu kubwa sana. Lakini tunashuhudia kwamba tunakwenda kupata CSR ambayo itakwenda kusaidia sana maeneo muhimu. Kwa mfano, tunakwenda kunufaika na ujenzi wa hospitali ambayo itajengwa katika eneo hilo, tunaenda kunufaika na ujenzi wa bwawa kubwa litakaloenda kujengwa eneo hilo, na pia kuna ujenzi wa shule ambao tunarajiwa utafanyika katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, yako mambo mengine mengi ambayo tumekaa kwa pamoja na mikakati imeshaanza kusimamiwa na Mheshimiwa January kuhakikisha kwamba miradi hii inayokwenda kusaidia wananchi inaanza kufanya kazi vizuri; haya ni manufaa makubwa ambayo tunaenda kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na changamoto kubwa ya kukatika umeme katika Wilaya yetu ya Kishapu; na kwa sababu tuna Mgodi wa Almasi wa Mwadui, lakini tuna migodi katika Mkoa wetu wa Shinyanga, kwa maana ya migodi iliyopo Wilaya ya Kahama. Haya matatizo ya kukatika kwa umeme baada ya suluhisho hili mimi naamini kwamba sasa tunaenda kuondokana na changamoto hizo. Na kwa hali hiyo ninaomba nikutakie kila la kheri ili usimamizi katika utekelezaji wa mradi huo uende vizuri na manufaa tuyaone kwa ajili ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie eneo la REA. Wilaya ya Kishapu mpaka sasa kwa mwaka wa fedha huu ambao tunakwenda kumalizia tumeweza kuwasha vijiji 13, na hii kazi imesimamiwa na SUMA JKT. Kwa hiyo, nawapongeza sana kwa jitihada kubwa ambayo wamekwenda nayo.

Mheshimiwa Spika, lakini bado tuna vijiji 28 kati ya vijiji 51 ambavyo vilikuwa havijapata umeme; vijiji 28 bado havina kabisa umeme. Kwa hiyo, naomba kasi hii iweze kuongezwa, na SUMA JKT chini ya Engineer Meja Mohammed nawaomba waongeze kasi ili suala la kuwasha umeme katika maeneo haya yaweze kuafanyika. Nimeshuhudia nguzo zimesambazwa katika vijiji vyote na tulikuwa tunasubiri nyaya ndiyo changamoto kubwa. Naamini kwamba kama hili nalo litasimamiwa maeneo haya yote yanaweza kupata umeme kwa wakati. Mimi naomba sana SUMA JKT muongeze kasi ili mradi suala hili liweze kukamilika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tu niyataje baadhi ya maeneo ambayo hayana kabisa, ni kata ambazo hazina kabisa umeme, ambazo ni Kata za Lagana, Mwasubi, Mwamashele pamoja na Bunambiu. Hizi ni kata nne ambazo hazina kabisa umeme. Kwa hiyo, nilikua naomba hata mkandarasi atazame kwa macho maeneo haya muhimu na hasa ile Bunambiu na Mwasubi kwa sababu ni maeneo ambayo maji yanapita mengi na ikifika nyakati za masika inawezekana changamoto ikawa kubwa sana, hivyo waongeze kasi kuhakikisha kwamba wanaharakisha katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ninaomba nipongeze sana kwa jitihada kubwa ambazo Mheshimiwa Waziri umekuwa ukisimamia suala zima la mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Tumeshuhudia kabisa kwamba sasa imefikia asilimia 80. Kazi hii ni kubwa unayoifanya; na mimi naomba nipongeze hata Kamati yenyewe ya Nishati kwa namna ambavyo mnasimamia kuona kwamba mradi huu unakamilika kwa wakati na hivyo Taifa liweze kuondokana na changamoto ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala zima la vitongoji, nina zaidi ya vitongoji 145 katika Wilaya ya Kishapu. Vitongoji ambavyo tayari vimeshapata umeme ni vitongoji kama 55, vitongoji zaidi ya 90 bado vina changamoto kubwa ya umeme. Pamoja na kuongezewa idadi hii ya vijiji 15 ambao ni mpango ambao unakwenda kutekelezwa lakini bado jitihada zinatakiwa ziongezewe ili kuhakikisha kwamba vitongoji vyote vinapata umeme. Maeneo haya Watanzania wamekubali kubadilika, na kasi ya wananchi wanavyojitokeza kujisajili kwa ajili ya kuwekewa umeme ni mkubwa sana. Ninaomba Serikali, kwa maana ya Wizara, Mheshimiwa January ongeza kasi ili vitongoji vyote tuweze kupata umeme kabla ya mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa namna ya pekee, sasa naomba nizungumze mambo machache ambayo ni changamoto nikishauri kwamba tuweze kusaidia katika maeneo haya. La kwanza, ni eneo la usafiri. Jimbo la Kishapu na Wilaya ya Kishapu ina tatizo kubwa la usafiri, lakini la pili ni watumishi, naomba eneo hilo na lenyewe litazamwe. Tuna tatizo kubwa la watumishi katika eneo hili; panapotokea emergency tatizo linakuwa ni kubwa sana kwa ajili ya kutatua matatizo ya aina hii.

Mheshimiwa Spika, ninakushuru sana kwa kunipa nafasi naunga asilimia mkono hoja 100, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. BONIFACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nami naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu kabisa ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Kalemani pamoja na Naibu Waziri wake, niwapongeze pia na watendaji wote katika Wizara hii. Sababu kubwa kwa nini nampongeza Mheshimiwa Kalemani ni kwa namna ambavyo amekuwa mfano wa kuigwa kwa Mawaziri na hasa katika jambo kubwa la kutusikiliza sisi lakini pia kufika kwa wakati katika majimbo yetu na kuona changamoto na matatizo yaliyopo katika maeneo yetu. Kweli wewe ni kiongozi wa kuigwa na Mawaziri wengine ningependa waige mfano na mwenendo wa Kalemani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kishapu ina jumla ya vijiji ya 127 lakini vijiji 75 vina umeme na vijiji 52 bado vina tatizo kubwa la umeme. Hivi navyozungumza kata tano hazina kabisa umeme kati ya kata 29 hata Kata nakotoka ya Lagana. Kata hizo ni Lagana, Bunambiu, Mwasubi, Itilima na Masanga, hizi kata hazina kabisa umeme hata katika kijiji kimoja. Kwa hiyo, hili bado ni tatizo kubwa sana katika eneo langu. Naomba sana Wizara katika hii REA III Awamu ya Pili vijiji hivi vyote viweze kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri mwaka 2017 aliweza kufika katika Jimbo la langu katika Kata za Ukenyenge, Mwamashele na bahati nzuri aliahidi kwamba maeneo hayo yatapatiwa umeme. Kata ya Mwamashele nguzo zimefika lakini mpaka sasa hatujapata umeme, kwa hiyo, bado wananchi wanasubiri umeme. Mimi ninahakika kwa jinsi ambavyo Waziri ameahidi atakwenda kutekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto kubwa ya kukatika umeme katika Mji wa Munze ambao ni Makao Makuu ya Wilaya yangu ya Kishapu, liko tatizo kubwa na kwa kweli jambo hili linasikitisha. Pengine wakati una-wind up naomba ueleze tatizo ni nini kwa sababu maelezo yako mengi. Kwa kutwa nzima umeme unapatikana kwa wastani wa asilimia 30 ama 40 asilimia 60 unakatika; kwa siku unaweza ukakatika mara tatu, mara nne ni tatizo kubwa sana. Tunaomba kujua tatizo ni ni linalosababisha kukatika kwa umeme katika maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nizungumzie ni masuala mazima ya watumishi. Wilaya ya Kishapu tuna watumishi 12 peke yake na Mheshimiwa Waziri anafahamu watumishi katika sekta hii muhimu ni kubwa. Pale inapotokea emergency, kwanza katika emergency gang inatakiwa watumishi 12 waende haraka kwa ajili ya kutatua tatizo sasa unapokuwa na watumishi wilaya nzima 12 panapotokea emergency unafanya nini pia kuna maeneo yanayotakiwa kutolewa huduma za kila wakati, kwa hiyo, hili ni tatizo kubwa.

Mheshimiwa Spika, pia nizungumzie suala zima la wakandarasi. Nchi nzima wakandarasi wametolewa katika kila wilaya, Wilaya ya yangu ya Kishapu haijapata mkandarasi, hili ni tatizo sijajua sababu ni nini. Wakati Mheshimiwa Waziri ana-wind up aeleze nini tatizo. Nimeendelea kufuatilia mchana huu Mkoa mzima wa Shinyanga hatujapata wakandarasi. Kwa hiyo, hili bado ni tatizo na pengine nataka nipate majibu tatizo ni nini. Juzi Waziri alisema atakapowaita hao wakandarasi pamoja na mameneja wa TANESCO kutoka katika kila wilaya atawapa maelekezo wawasiliane na Waheshimiwa Wabunge ili waweze kuona maeneo gani ambayo yana changamoto na ya kufanyia kazi kwa haraka, kwa hiyo, kwangu hili ni tatizo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie pale panapotokea matatizo ya moto. Mwezi Machi palitokea tatizo la kuungua nyumba tatu katika Kata ya Mwaweja Wilayani kwangu Kishapu kutokana na short za umeme. Tumepata tatizo kubwa sana kuzima moto katika nyumba zile lakini pia hata TANESCO wenyewe kuwahi kufika ilikuwa ni tatizo kubwa. Tatizo hili limechangiwa pakubwa sana kutokana na kutokuwa na magari na watumishi wa kutosha. Kwa hiyo, naomba sana mjaribu kuitizama Kishapu na watusaidie ili tuondokane na tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu kabisa Wizara ya Kilimo ambayo hotuba yake kimsingi ni hotuba nzuri na unaweza ukaona bajeti hii ni kubwa, ni takribani mara tatu zaidi ya bajeti katika kipindi kilichopita ambayo ina jumla Shilingi Bilioni 751. Kwa kweli naomba nitumie fursa hii kukupongeza sana Mheshimiwa Waziri Bashe, Naibu Waziri Mavunde, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu, Mrajisi wa Vyama vya Ushirika na Ndugu zetu Watendaji Wakuu, Bodi ya Pamba, Bodi ya Korosho, Wakurugenzi ambao kwa kweli mmekuwa mkitekeleza wajibu wenu pakubwa sana pamoja na watumishi wote wa Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kwa kweli kumshukuru sana na kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano, Mama yetu mpendwa Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaipa kipaumbele sana Wizara hii ya Kilimo ili mradi kuona kwamba Watanzania sasa wanapata ukombozi kupitia shughuli kubwa kwa sababu Watanzania zaidi ya asilimia 70 ni wakulima, tuna matumaini watanzania Mama atatufikisha pale ambapo sote tunatarajia tutakwenda kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo kimsingi nataka nianzie katika eneo zima la Wizara ambayo imefanya kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba wanatoa vitendea kazi hususan pikipiki kwa maana pia vifaa kwa ajili ya kupima udongo na vifaa vingine ambavyo kwa kweli vitasaidia sana kusukuma jitihada za mafanikio katika sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili Mheshimiwa Bashe pamoja na Naibu Waziri pamoja na Watendaji wote Wizara hii, ninawapongeza sana kwa ubunifu mkubwa na mawazo chanya ambayo nchi yetu ya Tanzania tunao uhakika kwa Watendaji kama hawa na Viongozi kama hawa tutafika mbali sana. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine muhimu sana ni kuhusiana na suala la pembejeo. Tumeshuhudia na hasa katika eneo ambalo ni la ukanda wa Ziwa Viktoria na hasa Mkoa wa Shinyanga na sisi tunalima zao la pamba. Tumepata pembejeo kwa maana ya viuatilifu pamoja na mbegu kwa wakati. Hili ni jambo kubwa sana kwa sababu kwa miaka mingi tumekuwa tukipiga kelele kuhusiana na suala zima la kuchelewesha mbegu na kuchelewesha dawa. Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia Suluhu Hassan na chini ya Mheshimiwa Hussein Bashe ukweli umeupiga mwingi na tumepata dawa kwa wakati na mbegu kwa wakati na wakulima wamelima kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa iliyopo ni suala la mvua. Wenzangu wamezungumza hapa, tuna mvua za wastani na kwa kipindi hiki hasa cha mwaka wa kilimo msimu huu, kwa kweli tunatarajia mapato yetu ya uzalishaji kupungua kutoka asilimia tuliyokuwa tunatarajia hadi asilimia 50. Kwa hiyo, tunaona kwamba kuna uwezekano wa zao la pamba kutokupatikana katika matarajio tuliyokuwa tumejiwekea kwa sababu ya hali halisi ya hewa na kutokana na suala la mvua kutokuwepo ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba jitihada hizi ziendelee katika msimu unaokuja ili changamoto hii isije ikajirudia kwa mara nyingine kabisa kuhusu suala la pembejeo na mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka nizungumzie jambo jingine ni suala zima la Kitengo cha Ushirika. Kuna changamoto kubwa katika eneo hili. Kwanza ni upungufu wa watumishi katika eneo hili. Kama tunavyofahamu Maafisa Ushirika hawa ndiyo Wakaguzi wa Ndani (Internal Auditor) katika Vyama vya Msingi katika maeneo yetu yote. Tatizo hili ni kubwa, unaweza ukaangalia katika Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu tuna Maafisa Ushirika Wanne, lakini Kishapu ina vijiji zaidi ya 128. Hili ni tatizo kubwa, Tarafa Tatu ukubwa zaidi ya kilomita za mraba karibu 4,300, ni eneo kubwa sana. Sasa Maafisa Ushirika Wanne, Vyama vya Msingi zaidi ya 98 watafanyaje kazi? Kwa hiyo, eneo hili tunaomba sana Mheshimiwa Waziri lifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ni suala zima la ku-over stay kwa watumishi. Maafisa Ushirika wapo ambao wanao umri wa miaka 15 mpaka zaidi ya miaka 15. Serikali na Wizara ifanye kazi ya ziada kuhakikisha kwamba watumishi hawa wawe wanahamishwa ili tuweze kuleta watumishi ambao wanaweza wakaleta chachu na mafanikio ya haraka katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine ni suala la sekta ya umwagiliaji. Tunashukuru kwamba Serikali katika mwaka huu wa fedha wametenga fedha za kutosha. Naomba skimu ya kwangu ya Itilima, skimu ya kwangu ya Nyenze, Idukilo hizi zipewe kipaumbele na hasa ile ya Itilima ina zaidi ya hekari 2,000. Eneo hilo ni kubwa na ni zuri. Serikali ya Awamu ya Nne iliwahi kuleta Shilingi Milioni 200 na baadhi ya miundombinu iko sawasawa. Naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuwa una-wind up eneo hili uzungumzie ni kwa namna gani utaenda kutusaidia ili hizi skimu ziweze kukaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ni Vyama vya Ushirika. Tuna Chama Kikuu cha Ushirika – SHIRECU. SHIRECU hii ndiyo imezaa Chama Kikuu cha Mkoa wa Simiyu, lakini Bukombe na Ushirombo pia KACU. Chama hiki ni kama tumekitupa. Zaidi ya awamu tatu au miaka mitatu ama minne tumekuwa tukiomba ukomo wa bajeti kwa ajili ya kuhakikisha tunafufua viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ginery ya Munze, wewe mwenyewe umefika Mheshimiwa Waziri Bashe na unaifahamu vizuri. Ginery ile ni nzima inahitaji matengenezo ya kawaida. Ginery ya Uzogole lakini tunayo Oil Milling Manispaa ya Shinyanga. Hizi asset tunazitupa, naomba Mheshimiwa Waziri, wameomba Shilingi Bilioni Sita. Shilingi Bilioni 4.4 ni kwa ajili ya ununuzi wa pamba pamoja na marekebisho ya magari, Shilingi Bilioni 1.3 kwa ajili ya kulipa madeni na vitu vingine, kwa nini katika Shilingi zaidi ya Bilioni Mia Saba hii tusije tukawafikiria SHIRECU? kwa sababu wakati mwingine tunakatisha tamaa Viongozi wa Ushirika na watu wa Ushirika. Naomba wakati una-wind up uzungumze kuhusu ginery ya Munze, ginery ya Uzogole na suala zima la ukomo wa madeni hizi Shilingi Bilioni Sita tuweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nina imani na wewe kwa sababu utakwenda kusaidia, lakini nikupongeze kwa sababu baadhi ya Vyama vya Ushirika ambavyo vimesajiliwa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Butondo kengele yako ya pili imeshalia tayari.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nami naanza kuungana na wenzangu kwanza kukupongeza wewe Spika wetu wa viwango kabisa kwa namna ambavyo Bunge letu hili tukufu ambavyo umekuwa ukiliendesha kwa umahiri na busara ya hali ya juu sana. Hongera sana Mheshimiwa Spika, Dkt. Tulia Ackson. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo Rais huyu ameendelea kukonga nyoyo za Watanzania na hasa kwa kuhakikisha kwamba anaendelea kuwatua ndoo akina mama ambao wamehangaika kwa muda mrefu sana na tatizo kubwa la maji. Kwa kweli sisi Watanzania tunamtakia kila la heri na afya njema Rais wetu aendelee kutuletea maendeleo katika Taifa letu hili la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Aweso pamoja na Mheshimiwa Mahundi, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na DG wa RUWASA kwa namna ambavyo kwa kweli wamekuwa wakitusimamia vizuri sana katika eneo hili la sekta ya maji. Watanzania wote wanaiona kasi yenu, utendaji wenu na kwa kweli sisi kama Wabunge, tunaridhishwa sana kwa namna ambavyo mmekuwa mkishirikiana na watendaji wa ngazi za chini, na pia kwa namna ambavyo mnashirikiana nasi Wabunge katika maeneo yetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumpongeza Engineer wetu wa Mkoa wa Shinyanga, Dada Juliet Kayovela, na pia nimshukuru sana Engineer wangu Dickson Mazima, huyu ni Meneja wa TARURA wa Wilaya ya Kishapu. Hawa wote kwa kweli wamekuwa na ushirikiano mkubwa nasi Wabunge na hasa mimi mwenyewe katika eneo la jimbo langu na watendaji wa Halmashauri na viongozi wengine katika Wilaya yangu ya Kishapu.

Mheshimiwa Spika, na hiyo unaweza kuona kwamba miradi katika Wilaya ya Kishapu imekuwa ikienda vizuri sana, lakini kwa sababu ya ushirikiano mkubwa wa RM pamoja na DM katika eneo langu hili la Kishapu.

Mheshimiwa Spika, nataka tu niseme kwamba mpaka sasa Kishapu tangu mwaka 2020 mpaka hii 2023, hali halisi ya upatikanaji wa maji ilikuwa ni asilimia 39 katika kipindi cha mwaka 2020, lakini kwa sasa tuko asilimia 76. Ni hatua kubwa sana. Hili ni jambo ambalo wengi wa wanaKishapu wanaona ni ndoto, ni jambo ambalo hawaliamini katika macho yao. Pongezi zote tunaomba tumrudishie Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuwa kweli Mama anaona umuhimu wa kuweza kuwasaidia na kuwashusha ndoo akina mama wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuna miji kama Maganzo inapata maji ya Ziwa Victoria, kuna Mbiu, Kata ya Mwadui Lohumbo, kuna Uchunga, kuna Wela, Ukenyenge na Mji wetu ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Kishapu, haya maeneo tunapata maji ya Ziwa Victoria, lakini haitoshi. Ipo miradi ambayo sasa hivi inaendelea kutekelezwa. Naomba tu nitaje baadhi ya miradi. Upo mradi wa Nyenze – Mwang’oro hadi Kabila; na Idukilo - Igumandobo ambayo ina thamani ya Shilingi bilioni 2.5. Mradi huu unaendelea mpaka sasa, na huu ni mradi wa maji ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, upo Mradi wa Ipeje – Itilima - Ikonopyelo, Ikoma na Ipeja. Huu ni mradi mkubwa wa thamani kubwa ya Shilingi bilioni 3.1, ni mradi ambao sasa hivi unaendelea pia kutekelezwa. Upo mradi wa Mwashohohela, huu ni uchimbaji wa visima; na Dulisi. Hii ni miradi ambayo inatekelezwa kwa sasa, japokuwa kuna changamoto ya upatikanaji wa maji, lakini naamini kwamba tutawasiliana na Mheshimiwa Aweso ili katika usanifu utakaokuwa unaendelea, tuone namna ambayo tunaweza kuwaokoa hawa watu wa Kata ya Sekebugoro, na ikiwezekana tuongezewe bomba pengine kutoka Old Shinyanga, ilimradi tuongezewe uwezo wa kuweza kusambaza maji katika maeneo hayo, kwa sababu maeneo hayo yako karibu sana na Old Shinyanga.

Mheshimiwa Spika, vile vile upo Mradi wa Wela, Wila, Mataga na Mwanulu, ni mradi ambao unaendelea mpaka sasa hivi, na huu ni mradi mpya. Hii ni miradi ambayo inakwenda. Upo Mradi mkubwa wa Igaga - Mwamashele unakwenda Mwamanota unakwenda Lagana, ni mradi mkubwa wa shilingi bilioni 6.5. Kampuni ya Emirates mpaka sasa ninavyozungumza iko site inaendelea na kazi. Ni mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, uko mradi wa Ndoleleji wa Malasa, Mwakipoya wa bilioni 1.6 mradi wa maji, usambazaji wa maji katika Mji wa Maganzo milioni 250 unaendelea. Lakini mradi wa usambazaji wa maji Mwamalasa, Mwamashimba mradi 101, pia kuna mradi wa Ngundangali – Seseko, mradi wa Mangu, Kiloleli, Ng’oloshinong’ela na Bulekela milioni 156 hizi tumeomba fedha za usanifu. Mheshimiwa Aweso tunaomba utupatie hizi fedha ili mradi tuone namna ambavyo tunaweza tukaamua ni mradi gani tutapeleka maeneo hayo. Kwa sababu uchimbaji wa visima virefu inaonekana kama unashindikana, ikiwezekana tutaomba tuchimbiwe mabwawa katika maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa Momolasa, Somagedi, Mwagalankulu ambao huu na wenyewe nimeuzungumzia lakini mradi wa Nobora, Jijongo milioni 510 unaendelea. Mradi wa kutoka Mhunze kwenye Mwabusiga na wenyewe unaendelea. Kwa sababu muda hautoshi naomba nizizungumzie baadhi ya changamoto, miradi wa Maji ambayo inafadhiliwa na Mfuko wa Maji wa Taifa imekuwa na changamoto kubwa, fedha zimekuwa hazifiki kwa wakati na hii imesababisha kuchelewesha miradi mingi ambayo iko chini ya mfuko wa fedha hizi. Mheshimiwa Waziri nakuomba sana hili jambo waone umuhimu wa kuweza kufatilia ili mradi mfuko huu utoe fedha kwa wakati na miradi iweze kutekelezeka kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo kubwa, kuna changamoto pia ya gari juzi nimepewa na Eng. Julieth gari moja kukuu nina gari moja lililochoka sana. Kwa hiyo, hili ni tatizo kubwa. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri kwa Wilaya ya Kishapu tupatie gari jipya ili mradi kazi ziweze kutembea sawasawa.

Mheshimiwa Spika, kuna suala zima la certificate zinapokuwa zimekuwa–raised na ziko tayari tatizo kutokutoa, kutokulipa fedha kwa wakati. Kwa fedha ya miradi yote hili limekuwa ni tatizo sugu nakuomba Mheshimiwa Waziri hili lisimamie hili certificate zinapokuwa raised na zilipwe kwa wakati ili mradi miradi iweze kutekelezeka kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ni maeneo ambayo…

SPIKA: Mheshimiwa Kengele ya pili imeishagonga, dakika moja malizia.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Maeneo mengine ambayo nilikuwa nataka kuzungumzia ni maeneo ambayo hasa ya miradi ambayo ni ya zaidi ya bilioni moja. Kumekuwepo na tatizo kubwa sana kwenye msamaha wa kodi VAT exemption. Ninaomba Mheshimiwa Waziri miradi mingi sana imekuwa ikichelewa kutekelezwa kwa sababu ya ucheleweshwaji wa upitishaji wa hii VAT exemption. Ninaomba sana hili lizangatiwe na hii itasaidia sana miradi kukamilika kwa wakati lakini hata wakandarasi hawa tuwahurumie wakati mwingine tunaingiza katika mufilisi pasipo kuwepo na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo baada ya kuzungumza hayo ninaunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu kabisa. Kwanza naomba nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mheshimiwa Rais ameendelea kuchanja mbuga kuhakikisha kwamba shughuli za kimaendeleo katika sekta zote zinakwenda kwa kasi kubwa na tumeshuhudia juzi zoezi la kusaini mikataba ya ujenzi wa minara na sisi Wabunge tumeshiriki na wadau wengine. Kwa kweli shughuli ile Watanzania wote wameiona kwa macho na ina kwenda kuongeza kasi ya upatikanaji wa mawasiliano katika Taifa letu la Tanzania kwa ujumla. Kwa hiyo tunaendelea kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada kubwa anazozifanya katika sekta hii muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwapongeze sana Mheshimiwa Nape, Waziri pamoja na Naibu Mheshimiwa Kundo…

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. BONIPHANCE N. BUTONDO:…kwa jinsi ambavyo wameendelea kushiriki pakubwa sana kuhakikisha kwamba…

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja…

NAIBU SPIKA: Husikiki, microphone yako imekaa vibaya. Mic yako ina nini, ina glitch?

(Hapa kipaza sauti hakikufanya kazi)

MHE BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshindwa kumsikia vizuri, lakini kwa ajili ya kulinda muda, naomba kulinda muda wangu, lakini kimsingi naamini atakuwa anazungumzia suala la muhimu sana la mawasiliano hasa katika Jimbo lake la Igalula na mimi ni mdau wa shughuli za maendeleo katika Jimbo la Igalula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, naomba pia niwashukuru watendaji wote katika Wizara hii kwa namna ambavyo wanafanya kazi zao vizuri. Sasa la pili nataka nizungumzie suala zima la minara; tumeshuhudia utiaji wa sahihi wa ujenzi wa minara 758, lakini 304 ambayo inaenda kuongezewa nguvu. Zoezi hili muhimu linaenda kuleta tija na kuharakisha shughuli za kimaendeleo kwa ujumla katika Taifa letu. Suala la mawasiliano ambalo lilikuwa linahangaisha hasa katika Jimbo la Kishapu, tunakwenda kunufaika pa kubwa sana kutokana na zoezi hili la kusaini mikataba ambalo limefanyika hivi karibuni. Katika hili narudia kumpongeza Mheshimiwa Rais, lakini tunakubaliana wote kwamba Sekta hii ya Mawasiliano ndiyo chachu kubwa ya maendeleo katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie katika maeneo haya ambayo yanaenda kunufaika na suala zima la minara hii. Mimi naenda kupata jumla ya vijiji 17 ambavyo vinaenda kupata manufaa na minara hii na minara hii iko minara 11. Hii ni pamoja na Busangwa mnara mmoja, Itilima ambayo ina Ikoma, Ileberebe na Mwajiginya B, lakini kuna Masanga pale panaitwa Dodoma, lakini kuna Mwakipoye Iboje na Mwakipoya yenyewe lakini pia na Shagihilo ambapo kuna Kijiji cha Mangu lakini kuna Mwamalasa ambapo Magalata wanaenda mnara, lakini Talaga ambayo ina Jijongo na Nendeghese inapata mnara. Pia maeneo haya yatakwenda kusaidia vijiji vyote jirani kupata mawasiliano kwa urahisi. Kwa hili namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Kundo kwa sababu alifanya ziara katika Jimbo langu na haya maeneo aliweza kuyabaini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kumwomba Waziri kwamba, maeneo ya Kata ya Seke Bugoro, Somagedi, Mwasubi na Bunambiu bado yana changamoto ya mawasiliano. Niombe sana katika kipindi cha mwaka wa fedha ujao, waweze kufanya consideration katika maeneo haya na yenyewe yaweze kupata mawasiliano kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nilizungumzie hapa ni suala zima la redio yetu ya TBC. Jukumu la TBC na hata katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumza kabisa wazi, ya kwanza ni kuhakikisha kwamba tunaielimisha jamii, kuihabarisha jamii lakini kuiburudisha jamii lakini na kuitafakarisha kwa kuzingatia kauli mbiu ya ukweli na uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kauli mbiu hii ya Ukweli na Uhakika lakini ikiwa ni pamoja na kuhabarisha, kuelimisha lakini na kuburudisha, bila mawasiliano ya uhakika ama bila usikivu wa uhakika, Watanzania wengi wanakosa mambo haya ya muhimu. Kwa hiyo naomba sana katika Jimbo la Kishapu maeneo makubwa sana Redio TBC haisikiki kabisa katika maeneo hayo. Niombe sana hili jambo liweze kufanyiwa kazi ili mradi wananchi wangu waweze kunufaika na redio hii muhimu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, tumeona kabisa katika mwaka wa fedha 2022/2023, fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba redio hii inasaidiwa na inakuwa na uwezo mkubwa wa kuhabarisha na kutoa taarifa zake, zilikuwa ni zaidi ya 13,133,000,000 lakini pesa ambazo ziliweza kupokelewa pekee yake zilikuwa ni bilioni 3.9 ambayo ni kama asilimia 30, unaweza ukaona kwamba ni fedha kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ione umuhimu wa kuhakikisha kwamba redio hii katika kila tengo la fedha zinazotengwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba redio hii inapata ufanisi, umuhimu huu tuuone kwa sababu wananchi wetu wanaenda kunufaika pakubwa sana sana. kwa hiyo nataka niiombe sana na niirai sana Serikali katika eneo la bajeti, utekelezaji wa upelekaji wa fedha zinakuwa zinatengwa katika kila mwaka wa fedha, ziwe zinapelekwa kwa asilimia 100 ili Mheshimiwa Nape, Naibu Waziri wake pamoja na watendaji wake sasa waweze kuona ufanisi na mafanikio ya bajeti inayotengwa katika kila kipindi cha mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala zima la uandishi wa habari, waandishi wa habari wengi sana jamani wamekuwa wana shida, huwezi ukasema ni omba omba japokuwa lugha ile sio nzuri. Tabu kubwa ni mikataba kwa watumishi hawa. Waandishi wa Habari hawana mikataba, wamekuwa wana shida kweli. Maisha yao kama si sisi wanapokuwa kwenye majukumu hayo kutowajali na kuwapa chochote, wanaishi maisha ya tabu sana. Tunaomba hawa Waandishi wa Habari kwa sababu Waziri ni baba na mlezi, awatazame na kuhakikisha anawalea na kuhakikisha kwamba waajiri hawa wana mikataba. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la msingi ambalo nataka nilizungumzie…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Butondo kengele ya pili, malizia sekunde mbili.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, ooh! Ninaunga mkono hoja, napongeza sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Teknolojia ya Habari kwa ujumla. Kwanza ninaomba nimpongeze Mheshimiwa Nape pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri Engineer Kundo kwa namna ambavyo Wizara hii wanaisimamia kwa karibu sana, wote tunashuhudia utendaji wao wa kazi kwa karibu na mimi ninawatakia kila la kheri na sisi wa Kishapu tutaendelea kuwaunga mkono kuona kwamba jitihada na juhudi mnazozifanya tunapeana ushirikiano wa karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni jambo zima la uanzishwaji wa kitengo cha mawasiliano ambacho kimeanzishwa na Wizara hii na mwezi wa Julai nadhani kinatarajia kuanza rasmi. Kwanza, niwapongeze kwa sababu ni utaratibu mzuri tumeshuhudia kupitia Msemaji wa Serikali Ndugu yetu Msigwa upashanaji na utoaji wa habari kwa umma umekuwa wa hali ya juu na watanzania wamekuwa wakielewa nini Taifa linatekeleza majukumu yake katika masuala mbalimbali Mtambuka. Sasa jambo hili ni jambo la muhimu sana lakini kitu ambacho ninataka nichangie ni kuhusiana na upungufu, ama uhaba wa watumishi hasa katika eneo hili la Kitengo cha Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu katika Halmashauri zetu 185, Halmashauri 100 peke yake ndizo zina Wakuu wa Idara hii ama Wakuu wa Vitengo hivi, Halmashauri zaidi ya 85 mpaka 86 hazina wakuu hawa wa vitengo hivi. Kwa hiyo, hii ni changamoto kubwa, kama Wizara ina dhamira ya dhati kuhakikisha kwamba vitengo hivi vifanye kazi zake vinavyotarajiwa kwa uhakika, haiwezekani kama hatutafanya jitihada za haraka sana kuona kwamba suala la kuhakikisha kwamba watumishi hawa wanajitosheleza katika Halmashauri linafanyiwa kazi haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo, ushauri wangu Wizara ifanye kazi ya ziada na kwa haraka zaidi kuhakikisha kwamba watumishi hawa wanajitosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba kwa sababu katika Halmashauri tuna baadhi ya watumishi ambao fani zao ama wamejiendeleza katika eneo hili la Habari, kuna haja ya kufanya recategorization katika Halmashauri zetu kwa haraka zaidi ili Watumishi tulionao katika ngazi za Halmashauri waweze ku-cover maeneo haya ambayo yana matatizo na mapungufu ya aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna haja ya kufanya recategorization katika Halmashauri zetu kwa haraka zaidi ili watumishi tulionao katika ngazi za Halmashauri waweze ku-cover maeneo haya ambayo yana matatizo na upungufu wa aina hiyo. Kwa hiyo, nilikuwa naishauri sana Wizara iliangalie hili kwa mapana ilimradi lifanyiwe kazi kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kwa sababu, tunaye msemaji wetu, kama nilivyozungumza Ndugu Msigwa na amekuwa akifanya kazi kubwa sana, nashauri ifanyike jitihada kubwa ya Wizara kuhakikisha kwamba inatoa mafunzo ya kutosha kwa hawa Maafisa Habari ili nao wawe na uelewa wa kutosha na waweze kuwa wanatoa taarifa hizi katika ngazi za Halmashauri kwa wakati ili Umma wa wananchi katika ngazi za Halmashauri wawe wanaelewa Halmashauri inatenda mambo gani na kwa wakati gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ipo changamoto kubwa ambayo nilikuwa nataka nishauri kuhusu nguvu ya kisheria, kwa sababu katika ngazi za Halmashauri wanaokuwa wasemaji katika ngazi za Halmashauri ni Wenyeviti wa Halmashauri na Wakurugenzi wa Halmashauri. Kwa hiyo, hawa wasemaji wanakuwa wasemaji tu labda katika mitandao ama wakati mwingine wanasimamia tu vitengo vile kwa ajili ya kutafuta Waandishi wa Habari ili waje wachukue habari katika mabaraza yetu. Kwa hiyo, sasa nilikuwa naomba Wizara iweke utaratibu na mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba inakuja na nguvu ya kisheria ili kuwapa mamlaka hawa wawe wasemaji katika Halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la mawasiliano na hasa simu. Kata ya Mwakipoya, Kata ya Mwasubi, Kata ya Masanga, Kata ya Somagedi, Kata ya Mwamalasa na Kata ya Itilima ni kata ambazo zina changamoto ya mawasiliano. Mheshimiwa Kundo aliwahi kuahidi kufika kwenye jimbo langu na kuja kuona changamoto hiyo. Kwa hiyo, kata hizi sita zina matatizo makubwa. Nilikuwa naomba sana kata hizi zipate huduma ya mawasiliano. Nimeona katika taarifa ambayo moja kati ya maeneo ambayo yanaenda kupata huduma hii, lakini maeneo haya bado yana changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, usikivu wa TBC bado ni tatizo kubwa katika Wilaya ya Kishapu. Naomba sana Wizara ifanye kazi kubwa kuhakikisha kwamba redio hii iwe inasikika kwa wananchi kwa sababu ni redio mama, na inatoa taarifa muhimu, mtambuka kwa ajili ya Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.2) wa Mwaka 2023
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, kimsingi nianze kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wetu wa Katiba na Sheria, ninamshukuru sana pia Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Pauline Gekul, ninamshukuru sana Attorney General na ninamshukuru Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati yetu kwa namna ambavyo amekuwa akiendesha vizuri Kamati hii na kutoa ushirikiano mkubwa na hasa tunapokuwa tunapitia mambo mbalimbali na hasa ya marekebisho ya Miswada mbalimbali katika Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami kwanza ninashukuru sana, nikianzia sehemu hii ya kwanza ya Atomic Energy, Cap. 188. Ukweli ni kwamba, jambo hili ni la muhimu na limekuja katika wakati muafaka, sote tunafahamu kwamba, ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba, afya za Watanzania zinalindwa. Eneo hili limekuja katika kipindi muafaka kwa sababu litakwenda kuhakikisha kwamba, baadhi ya mambo ambayo hatukuweza kujua ama jamii kutokufahamu sasa yanaenda kusimamiwa na kuzingatiwa kiasi kwamba, afya zao zitakwenda kuwa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza ninaamini kwamba, sote tunafahamu kwamba, itawezesha sana Tume kufanya kazi zake kwa ufanisi na hivyo hata utekelezaji wa majukumu yake unaweza ukawa unafanyika sawasawa. Pia tunaweza tukaona kwamba, kuna jambo ambalo linaenda kusaidia sana kupunguza athari za mionzi. Sote tunafahamu kwamba, mionzi imekuwa na athari kubwa, lakini tunajua katika hospitali zetu, kuna watumiaji wa vifaa mbalimbali ambao wanatumia vifaa hivi vya mionzi, lakini tumekuwa hatuwezi kudhibiti na kufuatilia kwa karibu kuona athari za mionzi hii. Kwa hiyo, sheria hii inaenda kusaidia sana kufanya ufuatiliaji na kudhibiti athari zinazoweza kujitokeza kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, tunaipongeza Serikali kwa sababu tunaona umuhimu wa afya za Watanzania wote kwa ujumla kwamba, ufuatiliaji na kuona hali ya udhibiti na matumizi yasiyokuwa yanafaa yanaweza kudhibitiwa.

Mheshimiwa Spika, kipengele kingine ambacho naenda kuzungumza ni kipengele cha kifungu cha 6(a) ambacho kinalenga kuanzisha Baraza la Taaluma katika chuo chetu hiki. Kimsingi hapa unaweza ukaona katika ushauri wa Kamati kwamba, kitakuwa chini ya Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Chuo, lakini tusiwe na mashaka kwa sababu timu ya wataalam akiwemo Makamu wa Chuo, Wakuu wa Idara mbalimbali, Mkuu wa Kitengo cha Sheria, Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi, Mlezi wa Wanafunzi, hawa wote ni wataalam ambao wanatosha kabisa kuifanya Bodi hii iweze kusimama vizuri na kuweza kutekeleza majukumu yake inavyopaswa.

Mheshimiwa Spika, kipengele hiki ni cha muhimu sana, nami nashauri kwamba, Waheshimiwa Wabunge tukubaliane kwa pamoja hii inaweza ikasaidia kufanya urahisi na pengine maamuzi kwa mfano ya mabadiliko ya kubalisha vifungu mbalimbali ambavyo vinaweza vikawa vinasaidia katika uendeshaji wa vyuo, inaweza ikasaidia sana maamuzi pengine kutekelezwa kwa wakati zaidi.

Mheshimiwa Spika, pia tunaweza tukaona kwamba, lengo la matumizi pia, I mean kuondoa hoja ya matumizi ya dola badala yake tuachie milango iwe wazi kiasi kwamba, matumizi ya fedha zozote zile zinaweza zikatumika, sote tunafahamu kwamba, malipo haya yamekuwa yakiwekewa masharti ya matumizi peke yake ya dola. Kwa hiyo, tukipunguza tukaondoa masharti haya itasaidia sana.

Mheshimiwa Spika, kuna jambo lingine ambalo tumeshauri kama Kamati kwamba, tuondoe neno council na badala yake tuweke bodi. Hii itasaidia sana, kukiwepo na bodi kama tulivyozungumza, bodi hii itakuwa imesheheni timu ya wataalam na wenye sifa mbalimbali, kwa hiyo, ufanisi ama marekebisho yoyote ya kikanuni ambayo yanaweza yakafanyika katika Bodi ama kubadilisha kanuni, yanaweza yakafanyika vizuri kwa sababu inakuwa na timu ya wataalam na wanataaluma wabobezi katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)