Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Paschal Katambi Patrobas (96 total)

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakubaliana kabisa na Serikali kwamba ina wajibu wa kulinda ajira za Watanzania kwanza, ndiyo priority. Hata hivyo, Sheria hii ya Uwekezaji sababu ya kutoa nafasi hizo tano automatic mojawapo ilikuwa ni hiyo trust ambayo mwekezaji anayo kwa wale watu watano bila kujali sifa walizonazo ni adimu au siyo adimu. Kwa mfano, watu wa finance mtu amewekeza mradi wake wa milioni mia moja in any way hata kama huyu mtu hana CPA…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Swali la kwanza, ni lini Serikali ita-harmonize hizi sheria mbili ili kutengeneza mazingira bora ya uwekezaji ili kuendana na kasi ya kuvutia wawekezaji nchini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa kwa sasa vibali vile life span yake ni ya muda mfupi mfupi na baadhi ya uwekezaji ni wa muda mrefu, je, Serikali iko tayari kuongeza life span ya vibali vile katika kuvutia wawekezaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza kuhusiana na mabadiliko ya sheria, mabadiliko ya sheria hufanyika pale tija inapoonekana. Katika mazingira ya sasa, Sheria ya Uwekezaji tuliyonayo, Sura 38, inatoa nafasi ya mwekezaji kuweza kupata watu watano kwa maana immigration quota. Watu hao watano wanapewa bila masharti yoyote, yeye ndiye atakayewachagua na hakuna hayo matakwa anayosema yapo kwa maana ya kuangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ni sehemu ya incentive au motisha. Katika kufanya hivyo, mwekezaji baada ya kuwa amekidhi vigezo vyote atakuwa na uhuru wa kuweka watu wake hao watano. Hiyo ni kwa mujibu wa Sheria ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa sheria inayohusiana na kuratibu ajira za wageni, yenyewe pia inatoa tu utaratibu na mwongozo mzuri wa local content katika kulinda uchumi wa nchi yetu lakini pia kulinda ajira za wazawa. Sasa katika mazingira haya ukiacha goli wazi, kwa sehemu kubwa uzoefu unaonyesha kila mwekezaji angependa kufanya kazi na watu ambao ni wa kutoka nje. Tuna taarifa kwamba wapo pia wawekezaji wanapata mikopo kutoka kwenye mabenki mbalimbali na masharti inakuwa ni kuajiri raia wa huko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Serikali yetu tunawekeza sana kwenye elimu, tuna mpango wa elimu bila malipo ambapo Serikali inatoa fedha nyingi katika sekondari lakini pia vyuo vikuu tunatoa mikopo, vijana hawa wanapomaliza vyuo na ajira hizo zikichukuliwa na wageni inakuwa ni changamoto kwa nchi. Ndiyo maana kwa ikatungwa sheria hiyo udhibiti ili kuhakikisha kwamba ajira za wazawa zinalindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake dogo la pili kuhusu life span ya permit, nimweleze tu Mheshimiwa kwamba nalo limezingatiwa vizuri na sheria za sasa zinatosha kabisa katika kuelezea hilo. Mwekezaji nchini mbali na kupewa idadi ya watu watano ambao wanaweza kufanya nao kazi, Sheria ya Uwekezaji inatoa muda wa kipindi cha miaka mitano lakini pia akiombea kupitia TIC anapewa kipindi cha miaka kumi. Katika miaka hii kumi na yule anayepewa miaka mitano imewekwa katika awamu ili kuhakiki na kujiridhisha kwamba kweli bado ajira hiyo ni adimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka miwili anapata permit yake ya kwanza ambapo atahitaji kuwa na succession plan aturidhishe kwamba kuna Mtanzania nyuma anajifunza kazi hiyo ya kitaalamu ili hata baadaye hata akiondoka nchini tuweze kubaki na wataalamu. Atapewa tena awamu ya pili miaka miwili na mwisho atapewa final grant kwa maana ya kufikisha miaka mitano. Mazingira hayo yote yanaangaliwa na wakati mwingine wamekuwa wakikata rufaa ofisi ya Waziri mwenye dhamana na zimekuwa zikitolewa kwa kupima mazingira yalivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mpaka sasa hitaji la kubadilisha sheria halijaonekana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka tu kuongezea kidogo kwenye majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Serikali pia ipo katika mchakato wa kufanyia marekebisho Sheria ya Uwekezaji. Pamoja na mambo mengine tutayaangalia baadhi ya mambo Mheshimiwa Mbunge ameya-raise hapa. Pia Waheshimiwa Wabunge watapata nafasi ya kuipitia sheria hiyo na kama kuna maeneo ya kuimarisha basi itakuwa ni fursa nzuri ya kuweza kurekebisha. Ahsante sana.
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini ninaa nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kati ya hao vijana 5,538 ambao wamepatiwa ufundi au mafunzo stadi ni wanufaika wangapi wanatoka Zanzibar?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, baada ya mafunzo hayo, je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwatafutia miradi ama fursa mbalimbali ili waweze kujiajiri na kuajirika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kuhusu swali la kwanza, nikubaliane nawe lakini pia mbali na takwimu suala hili limekuwa likifanywa na Wizara ya Michezo, Vijana na Utamaduni kwa upande wa Zanzibar. Kwa hiyo, tutapata takwimu hizo na tutaziwakilisha kwa sababu suala hili kwa upande wa Bara na Zanzibar kuna parallel program lakini zaidi tunashirikiana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, ni kweli kwamba vijana hawa wanapomaliza kupewa mafunzo na stadi za kazi wanazopewa, Serikali imeweka mpango katika mifumo miwili.

Kwanza, kuna Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambapo vijana hawa baada ya kupewa stadi hizi za kazi wanaweza kuwezeshwa katika hatua ya pili baada ya kuwa wamebuni miradi ambayo ni endelevu na ambayo inaweza ikawasaidia vijana kuweza kujikimu katika maisha yao lakini pia kuweza kufanya biashara au kuwekeza kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo kwenye sekta za kilimo. Kwa mfano, kwa kipindi cha mwaka wa jana katika halmashauri 84 yalitolewa mafunzo na kampuni tatu hizi hizi za vijana waliopata mafunzo na wakapewa fedha zaidi ya shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya kutoa mafunzo ya kutengeneza vitalunyumba ambapo zoezi hilo limefanyika katika halmashauri 84. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya pili fedha hizi za Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwenye halmashauri kwa maelekezo hayo hayo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wetu wa Nchi, Mheshimiwa Jenista Mhagama wamekuwa wakisimamia ambapo fedha zimekuwa zikitolewa na halmashauri kupitia 4:4:2 kwa maana ya asilimia 4 kwa wanawake, asilimia 4 kwa vijana na asilimia 2 kwa watu wenye ulemavu katika halmashauri zote. Fedha hizi zinakusudia kuwapa vijana mikopo au fursa ya kuweza kujiendeleza katika maeneo ambayo watakuwa wameendelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo katika eneo hilo hilo ni agizo la Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mpango ambao umewekwa kwamba katika Halmashauri zote yametengwa maeneo ya vijana kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watakapotaka kujiingiza kwenye kilimo au fursa zozote wanaweza wakapewa. Mathalani ukiangalia Kahama kuna eneo la Zongomela ambapo vijana waliopata mafunzo ya ufundi stadi wameweza kupata eneo lile na wanatengeneza samani mbalimbali ikiwemo grill, vitanda lakini pia wanauza mbao. Ukienda eneo la Mvomero vilevile kuna garage ziko pale zimetengenezwa hata maeneo ya Misungwi na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa kifupi tu nimwambie kwamba vijana hawa wanapopata stadi hizi za kazi bado hawaachwi hivi hivi tunaendelea tena kuwalea ili kuhakikisha kwamba zile stadi na skills walizozipata zinawasaidia katika kujikwamua kwenye maisha yao. Nashukuru.
MHE. AMINA D. HASSAN: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; pamoja na majibu yake mazuri Naibu Waziri aliyonipa, nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, ni lini hasa Serikali itaanza kulipa mafao ya wanachama ambao wana miaka zaidi ya mitatu wanafuatilia masuala yao hawajafanikiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, pili je, Serikali inamkakati gani kuhakikisha kwamba wastaafu wanalipwa kwa wakati ili isiathiri dhamani ya fedha ambayo wanalipwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge Amina Daud Hassan kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni lini Serikali itakamilisha ulipaji wa Wawanachama ambao wana miaka mitatu sasa ambapo hawajaweza kulipwa mafao yao. Nimakikishie Mheshimiwa Mbunge kwanza nimpongeze kwa kufuatilia hasa kuhusu wananchi wake katika matatizo hayo ambayo wanayapata labda pengine ya kuwacheleweshea malipo. Lakini zaidi niweze kumuambia Mheshimiwa Mbunge mpaka sasa mfuko wetu hauna madeni kwa maana ya kwamba wastaafu wote ambao wamewasilisha nyaraka zao zenye usahihi ndani ya siku 30 anakuwa ameshalipwa malipo yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwa kama kuna mwananchi wake ambao amewasema zaidi ya miaka mitatu pengine hawajaweza kulipwa mafao yao niombe tu niwasiliane naye, nipate hizo details ili niweze kushughulikia waweze kulipwa kwa sababu ni haki yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu mkakati wa Serikali wa kuhakikisha malipo haya yanalipwa kwa wakati. Tayari Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na kwa maelekezo yake, tumekwisha kuanza kufanya kazi ya kuchunguza madai, lakini pia kuweza kuangalia kwa undani tija ya fedha ambazo zinapatikana katika mfuko, zaidi ya hapo uwekezaji unaofanywa pia na mfuko na tatu tunaenda katika kufanya uchunguzi wa madai yote ambayo yalikuwa ya awali kama yapo kuweza kujihakikishia kwamba yanafanyiwa uchunguzi na baada ya kujiridhisha tuweze kuwalipa madeni hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika huo mkakati ambao upo mkubwa kwa sasa tunasubiri actuarial report ambao Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu amekua akiisimamia kwa kipindi chote na actuarial report itatoa taarifa kwa ujumla jinsi status ya mifuko hii na namna gani ambavyo itajiendesha kwa faida zaidi kama jinsi ambavyo Mheshimiwa Rais jana katika hotuba yake aligusia na kuweza kueleza namna gani ambavyo mashirika ya umma, lakini taasisi na mifuko iweze kujiendesha kwa faida. Kwa hiyo hili Mheshimiwa Mbunge, tunakuakikishia kwamba halitavuka miezi miwili tutakuwa tumekwisha kumalima kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu
Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Tumekuwa tukifanya uhakiki wa wastaafu kwenye mifuko hii, moja ya matatizo ambayo tumeyagundua ni hayo ambayo Mheshimiwa Naibu Spika umeayazungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wastaafu wamekua wakisumbuliwa sana kuleta nyaraka na wakati mwingine mstaafu anadaiwa alete nyaraka za miaka 20 iliyopita na wakati amestaafu nyaraka hizo zikiwa kwenye Ofisi za Serikali, tumeshatoa maelekezo kwa mifuko yote na hasa sheria inasema wajibu wa kufuatilia michango na nyaraka ni wamifuko na siyo mstaafu mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kazi yetu kwa sasa ni kusimamia watendaji wa hii mifuko wanatekeleza maagizo hayo tuliyoyatoa na kama kutakuwa na mstaafu anasumbuliwa yeye sasa ndiyo haangaike na ma-file wakati ni wajibu wa mwajiri na wajibu wa mifuko, tunaomba Waheshimiwa Wabunge tupeane taarifa na tutachukua hatua kwa hao watendaji ambao hawazingatii huduma bora. (Makofi)
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kwanza nisahihishe majibu ya Mheshimiwa Waziri. Jina langu siitwi Alice Kapungi, naitwa Alice Karungi. Baada ya hapo nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kutokana na umuhimu wa Sera hii ya Taifa ya Tija: Je, ni lini sera hii itakuwa tayari ili iweze kutumika tena kukuza tija? (Makofi)

Swali la pili, kutokana na marekebisho ya sera, sheria na kanuni ndogo ndogo za uwekezaji kwa nia ya kukuza uwekezaji: Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kukishika kikamilifu kitengo hiki katika marekebisho haya ya sheria ili mwisho wa siku sheria hizi ziwe zenye kuleta tija? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Alice Karungi Kaijage, kwa kipindi chote amekuwa akitupa ushirikiano mzuri sana katika kuhakikisha tunafanya maboresho kwenye maeneo mbalimbali hasa kwenye maeneo ya kazi, vijana na pia kwenye masuala mtambuka kama ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, swali lake la nyongeza, napenda kujibu kuhusu lini sera hii itakuwa tayari? Kwa hatua ya sasa tayari tumeshaanza kuchukua maoni kwa wadau. Bahati nzuri sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu ameliuliza swali hili, kuna uwezekano mkubwa kwamba ana ufahamu na uelewa mpana juu ya jambo hili. Namwomba pia awe sehemu ya hao wadau ambao tutawafikia kwa ajili ya kukusanya maoni hayo tukiwa tunaenda kukamilisha sera.

Mheshimiwa Spika, baada ya bajeti hii nina imani kwamba kwa mwaka huu 2021 tunaweza kwenda kukamilisha sasa uwepo wa sera na pia kuangalia mabadiliko ambayo tutayafanya katika sheria. Hili litatusaidia sana kwa sababu tumeliona kama Ofisi ya Waziri Mkuu litatusaidia kukuza tija na ubunifu katika maeneo mbalimbali. Kwa mfano, kwenye maeneo ya Agro-industry, automobile industry, airspace industry, mechanical industry, petro-mechanical industry na kwenye maeneo mbalimbali ambayo ni mtambuka.

Mheshimiwa Spika, viwanda vyetu na maeneo mengine hata ya kazi yamekuwa yakitengeneza bidhaa ambazo mwisho wa siku kunakuwa na uzalishaji mkubwa, lakini ubora unakuwa chini. Kwa hiyo, hili ni eneo muhimu sana ambalo Serikali tumeona tuliangazie pia.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Dkt. Alice kuhusu kukamilisha utaratibu wote wa mchakato wa kisheria kuweza kuhakikisha suala hili nalo linakuwa na nguvu ya kisheria ukiacha hivi hivi; hilo litaenda sambamba pamoja na hatua ya sasa ya kukusanya maoni ambayo tumekwisha kuianza na tuna imani kubwa kwamba kufikia mwaka huu tutakuwa tumekamilisha zoezi hilo na kuweza kurasimisha ili kuleta mapendekezo ya mabadiliko ya sheria, sambamba na kuwa na sheria ambayo inaweza ikasimama hapo.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu ya Serikali ambayo naweza kusema kwamba hayaridhishi. Kwanza ni-declare interest kwamba na mimi ni miongoni mwa waathirika, nimepoteza mali yenye thamani ya zaidi ya shilingi 301,516,000. Pia kuna nyumba zaidi ya sita zenye thamani ya shilingi 417,300,000; magari nane yenye thamani ya shilingi 299,700,000; pikipiki nane zenye thamani ya shilingi 22,100,000 na vifaa vya ndani vyenye thamani ya zaidi ya shilingi 145,169,000. Jumla uharibifu huu umeigharimu halmashauri yetu zaidi ya shilingi milioni 886.

Mheshimiwa Naibu Spika, waathirika, kama nilivyosema, mimi mwenyewe ni mmoja wao, lakini yuko Musa Mkoyage, Hassan Liwango…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka, hilo ni swali, uliza swali lako.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Sasa swali langu; hivi ni kweli Serikali pamoja na uharibifu huu mkubwa haioni umuhimu wa wananchi hawa waathirika zaidi ya 15 angalau kuwashika mkono? Ni kweli nchi yetu inaongozwa kwa sheria pamoja na kanuni, lakini kuna mila na desturi ya kufikiria kwamba hawa watu wameathirika, hawana mahali pa kuishi, hawana namna nyingine yoyote ya kushiriki maendeleo ya nchi hii; kweli Serikali haioni umuhimu wa kuwashika mkono watu hawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zuberi Mohamedi Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiri kwamba jambo lililofanyika siyo zuri na Serikali imelipokea kwa uchungu mkubwa. Kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema vizuri ni kwamba ni kweli nchi hii inaongozwa kwa mujibu wa sheria na sheria inayoongoza hapa ni Sheria ya Menejimenti ya Masuala ya Maafa ambayo ni ya mwaka 2015, yanapogeuka kuwa makosa ya jinai tayari inakuwa imeingia katika utaratibu mwingine. Ukisema ulipe fidia kwa watu ambao wamefanya uharibifu wa maji, kwa mfano, squandering of property, lakini pia kunakuwa na overt act kwa maana ya tendo ovu ambalo limekusudiwa, sasa tunaangalia ile mens rea na actus reus; kama tendo limefanyika ambalo kimsingi limevunja sheria maana yake hatua kali za kisheria lazima zichukuliwe kwa sababu ukilipa fidia kwa watu ambao wamefanya makosa maana yake tunachochea zaidi watu wengine kuleta madhara zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Amiri Jeshi Mkuu na vyombo vyake vya ulinzi na usalama wakati wa uchaguzi au maafa lakini pia wakati wa sherehe zote za Kitaifa na nyakati zote kuna timu ambazo zimeandaliwa, kuanzia ngazi ya kata tunazo kamati ambazo zinahusika na kufanya upembuzi wa kujua kwamba hili ni janga na ni afa ambalo linahitaji kuweza kuingia katika perimeters za Sheria hii ya Menejimenti ya Masuala ya Maafa. Pia kwenye ngazi ya wilaya, tunao Wakuu wa Wilaya ambao wanaongoza Kamati za Ulinzi na Usalama, ambazo ndizo timu pia za maafa kwa ajili ya kufanya ile assessment.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa suala hili lilivyojitokeza Liwale, moja kwa moja ni kosa la jinai. Kwa hiyo, hatua zitachukuliwa na kwa hatua ya sasa tayari evaluation imefanyika, nadhani tumeshauriana ameliona hilo, ni jinsi ambavyo tunataka sasa kuja kupata taarifa ya mwisho ya jinsi gani ambavyo madhara yalifanyika, watuhumiwa waliokamatwa na hatua kuchukuliwa zaidi ili kuweza kupeleka kesi zenye ushahidi mahakamani ili waweze kuwajibishwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kusisitiza wananchi wote kufuata sheria, taratibu na kanuni katika maeneo yao. Niseme tu hili, imekuwa ikijitokeza mara nyingi kwenye uchaguzi, watu wanaposhindwa hawakubali kwamba wameshindwa matokeo yake anataka kufanya justification ya kutaka kuonesha kwamba yeye alikuwa na nguvu kwa hiyo wanatengeneza matukio ya kihalifu. Kumekuwa na timu ambazo wanaleta vijana kwa ajili ya kufanya uhalifu huo. Serikali iko imara, vyombo vya ulinzi na usalama viko imara, navipongeza kwa hatua ambazo wamekwishaanza kuzichukua na ambazo tunaendelea nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii pia kupongeza Jeshi letu la Polisi katika kipindi cha uchaguzi limefanya kazi nzuri. Nipongeze Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, hata kwenye maafa haya lilihusika. Nipongeze pia vijana wa Scout lakini pia vijana wetu wa Red Cross ambao wamekuwa wakifanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. SANTIEL E. KIRUMBA: Mheshimiwa Spika, je, Serikali ina mpango wowote wa kuzigawanya fedha hizi katika Halmashauri hususan zile Halmashauri ambazo makusanyo yake yamekuwa madogo katika asilimia 10 ambazo zinatengwa. Halmashauri hizo mfano ni Wilaya yetu ya Shinyanga Vijijini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa nini Serikali isiongeze zile asilimia kutoka asilimia 10 mpaka tano kwa wanawake kutokana na wanawake wamekuwa ni watu wazuri sana katika marejesho? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali inayo mpango wa kuweza kufanya mapitio na kuweza kuweka maboresho zaidi kwenye mifuko hii kwa sababu ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya Halmashauri nyingine zenye kipato cha chini zile asilimia nne kwa wanawake, nne kwa vijana na mbili kwa watu wenye ulemavu kwenye maeneo mengine wanapata pungufu zaidi ya hapo. Kwa hiyo, hilo nalo ni jambo ambalo tumeshalichukua kama Ofisi ya Waziri Mkuu na limekwisha kuanza kufanyiwa vikao vya tathmini na kuweza kuangalia namna gani tutaweza kuboresha ikiwa ni sambamba na ule mjumuisho wa mifuko hii inayoshabihiana.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo lingine tumeona kwamba mikopo inayotolewa kwenye Halmashauri tunajaribu kuangalia zaidi tija, vikundi vimekuwa vikijiunga kwa ajili ya lengo la kupata mikopo ile, lakini baada ya hapo vinasambaratika na hawaendi kufikia azma ya kukopea mikopo hiyo na mpaka sasa tukisema katika mifuko tu ya fedha za Halmashauri ni mabilioni mengi ambayo bado hayajaweza kufanyiwa marejesho. Na kwa Ofisi ya Waziri Mkuu peke yake tuliwahi kutoa shilingi bilioni 4.9 lakini katika fedha hizo, ni shilingi milioni 700 tu ambazo ziliweza kurudishwa, zaidi ya shilingi bilioni nne bado hazijaweza kurejeshwa.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili Mheshimiwa Santiel Kirumba, Mbunge wa Viti Maalum kwamba kuona ongezeko la asilimia; hili ni eneo pia nalo ambalo tumekuwa tukilifanyia kazi kuweza kuona namna gani tunaweza tukaboresha Zaidi hasa kwa wale waliokuwa waaminifu katika kukopa kwa sababu lengo la Serikali na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ni kuwawezesha wananchi hawa kiuchumi wanapokopa hizi fedha waweze kuzirudisha ili watu wengine waweze kufanyia biashara zaidi. Na tunategemea waweze ku-graduate kwenye hilo eneo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kweli tunalifanyia kazi na tunatarajia hivi karibuni hasa kwenye mwaka huu wa fedha, fedha hizi zinazotolewa tuone ile tija na hasa twende hata kwenye kukopesha vifaa kuliko fedha ambapo mara nyingi zimekuwa zinatumika vibaya. Nakushukuru.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na nashukuru sana Serikali kwa majibu mazuri. Sasa nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali haioni ipo haja ya kufanya tathmini ya mifuko hii ya uwezeshaji kwa kuzingatia muda mfuko ulipoanzishwa, jumla ya mikopo iliyotolewa, ruzuku na dhamana pamoja na hali ya marejesho. Na tathmini hii pia iangalie hasara na faida ili kwa kufanya hivyo, Serikali iweze kuja na mikakati ya kuimarisha utendaji wake na iwe na tija kwa maendeleo ya wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili ni kutokana na changamoto kubwa za ajira kwa vijana, je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kuweka vipaumbele vya kutoa startup capital kwa wahitimu wa vyuo maana mara nyingi vijana hawa wanakuwa na bankable ideas lakini wanashindwa namna ya kupata mikopo, ruzuku na dhamana zenye riba na vigezo nafuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA
NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana kwa sababu amekuwa mfuatiliaji kwa wakati wote katika masuala haya yanayohusu maendeleo ya vijana lakini pia wanawake na Watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna haja kubwa ya kufanya tathmini ya muda kuhusiana na masuala ya ruzuku na dhamana ambazo zimekuwa zikitolewa kila wakati ili kuangalia kama inaleta tija. Katika hatua hiyo, Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa tayari tumekwishakuanza kufanya zoezi hilo ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya mifuko yote 54 na ile mitatu ambayo ipo chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu tayari tumekwisha kuanza kufanya zoezi hilo ili kuweza kuangalia namna gani ambavyo itakuwa na tija zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo ambayo baadhi ya hayo ambayo tumeyabaini, ukiacha kazi ya timu ambayo bado inaendelea, tumebaini kwamba katika fedha hizi nyingi zinatolewa wakati mwingine vikundi vinakuwa havijaunganishwa vizuri zaidi na tumeenda kwenye hatua ya kuona kwamba lazima sasa kuwe na tija ya kutoa mafunzo kabla ya kutoa mikopo hii. Vilevile kuweza kufanya na kuangalia yale maandiko ya mpango kazi au mpango wa biashara kwa maana ya zile business writeups ambazo zinazletwa kwa ajili ya wao kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hatua nyingine pia tunaangalia namna ya kuweza kutanua wigo wa kutoa mikopo hii au fedha hizi na uwezeshwaji huu kwa makundi mengi zaidi na kuona jinsi gani ambavyo inaweza ikaenda kwa mtawanyo kwa maana ya uwiano mzuri katika mikoa lakini pia katika Majimbo na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tumebaini jambo jingine ambalo katika mikopo hii ambayo imekuwa ikitolewa, na tutakubaliana kwamba fedha hizi zimekuwa zikitolewa katika mifumo mbalimbali. Ukiangalia kwenye Halmashauri kuna ile 4:4:2 kwa maana ya fedha ambazo ni asilimia 4 kwa wanawake, 4 kwa vijana na 2 kwa watu wenye ulemavu. Fedha hizi zimekuwa zikitolewa nchi nzima lakini kwa sehemu kubwa utaona kwamba marejesho yamekuwa ni hafifu sana. Kwa hiyo, tulitegemea kwamba fedha hizi zikitolewa, vijana hawa waweze kuzifanyia kazi na wa-graduate waende kwenye hatua ambayo watawaachia wengine waweze kukopa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaenda kwenye hatua nyingine ambayo bado ipo katika hatua ya mashauriano kuona kama tutaweza kutoa asilimia 50 ya vifaa na 50 iwe fedha kwa ajili ya operational cost kwa sababu ili tuweze kama ikitokea wameshindwa kulipa, tumewapa trekta au mashine za kushona nguo ama tumewapa vifaa vitendea kazi labda mashine za kufyatua tofali na ilikuwa mkopo labda wa milioni 10; tukawapa milioni 5 gharama za mashine na milioni 5 nyingine wakapewa kama fedha taslimu maana yake ni kwamba hata wakishindwa kurejesha walau tunaweza tukarejesha ile mashine ya kufyatua tofali ikawasaidie vijana wengine kuliko sasa hivi mfumo wa returns umekuwa mgumu na halmashauri zimekuwa zikihangaika wakati mwingine kulazimika kuwapeleka mahakaman. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la Mheshimiwa la kuona namna gani ambavyo tunaweza tukatengeneza startup capital kwa wanafunzi wahitimu wa vyuo vikuu ni pamoja na mpango mzuri ambao tumekuwa nao katika Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu…

MWENYEKITI: Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri utajibu hapo kwa ufupi.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA
NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Ni pamoja na mpango huu ambao tumeanza kuona bado lipo katika kuona namna gani ambavyo vijana wa vyuo vikuu tutawaingiza kwa programu tatu ambazo zipo. Kwa sasa tumeanza na programu ya uanagenzi ambayo kimsingi inatumika kwa wale ambao hawajamaliza chuo kikuu lakini tuna programu maalum ya internship ambayo tayari tunawachukua vijana hawa na kuwaunganisha kwenye maeneo ya ajira. Sambamba na hilo, tunatoa mafunzo pia na kuwasaidia kuweza kupata mikopo kwenye maeneo ya halmashauri lakini pia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana unaotolewa na Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo pia tumelichukua na tutalifanyia kazi, nakushukuru. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri yenye mikakati ya Serikali juu ya watumishi wao, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika Jimbo la Kibaha na majimbo mengi nchini kuna watumishi ambao wamechelewa kulipwa mafao yao kutokana na waajiri kutokupeleka michango yao kwa wakati. Je, Serikali inawasaidiaje watumishi hao, kwani waajiri wao wamefanya kinyume na utaratibu wa sheria?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kuanzia mwaka 2016 mpaka 2020, kulikuwa na maelekezo mbalimbali ya Serikali juu ya upandishwaji wa vyeo, kuna watumishi ambao wamestaafu wakiwa na barua mkononi lakini wameshindwa kulipwa kutokana na barua zao walizo nazo. Lakini pia kuna watumishi walichelewa kupandishwa vyeo kwa sababu ya waajiri kuwasahau kwenye kuingiza kwenye mfumo.

Je, Serikali inawasaidiaje watumishi hao ili waweze kupigiwa hesabu zao kulingana na haki na sheria ilivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Costantino, kwa kufuatilia vizuri sana haki za wananchi wake katika Jimbo la Kibaha Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la kwanza ambalo ameuliza ni utaratibu gani tunaochukua kwa wale waajiri ambao wanachelewesha michango lakini pia wanaosababisha fedha zile zisiweze kulipwa kwa wakati, hasa hizi za pensheni. Tumekwisha kuchukua hatua mbalimbali kwa mameneja wa mikoa wa PSSSF, lakini pia hata kwa NSSF kwenye maeneo ambayo tunagundua kwamba kuna uzembe wa ukusanyaji wa michango. Tumekuwa tukichukua hatua kali kwa wakurugenzi wa PSSSF Mikoa, lakini pia complying officers ambao tumekuwa tukiwaagiza kwa wakati wote watoe taarifa ya wadaiwa sugu kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu waajiri wanapochelewesha michango ni pamoja na kukwepa kodi, kwa sababu kuna PAYE kwenye mshahara wa mfanyakazi, kuna fedha inayopaswa kuinia katika Mfuko wa WCF, kuna fedha inayopaswa kulipwa kama Skills Development Levy, lakini vilevile kuna fedha ambayo ni ya mafao ya mfanyakazi, anapomaliza wakati wake wa kazi itamsaidia kwenye maisha yake. Kwa hiyo tunachukua hatua kali, na sheria inaelekeza na tumekuwa tuna kesi mbalimbali ambazo zinaendeshwa kwenye mahakama mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuagiza kwamba mameneja wetu wa mikoa na complying officers waweze kufuatilia michango.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili kwa kifupi, ni kwamba swali hili liko Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma, kwa wafanyakazi ambao ni wa Serikali. Nikuombe Mheshimiwa Mbunge, mimi pamoja na wewe tuweze kuiona ofisi ile na tuweze kufuatilia madai hayo ili waweze kupata haki na stahiki zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Utakubaliana na mimi kwamba tatizo la ajira kwa vijana kwa nchi hii limekuwa kubwa na la muda mrefu na Serikali ilishaji-commit, wakati nikiwa Mbunge wa Vijana kipindi kile wakati tunapitisha hapa Sheria ya Baraza la Vijana. Kwamba, kila Halmashauri itatenga maeneo ya kilimo kwa ajili ya vijana hasa ambao ni graduate waweze kwenda kujiajiri wenyewe. Lakini ardhi yenye rutuba ya daraja la kwanza, daraja la pili wamekuwa wakipewa wawekezaji. Hii ardhi ambayo vijana wanaitumia unakuta wamepewa na Mjomba, Shangazi na Bibi.

Je, lini Serikali mtatimiza ahadi ambayo mmeweka kutenga ardhi kwa vijana na kuwawezesha ili asilimia kubwa ya vijana waweze kujiajiri wenyewe? (Makofi)

Swali la pili; Serikali tulishatunga Sheria ya Baraza la Vijana na Vijana wanakosa chombo chao cha kujadili Kitaifa bila kujali itikadi zetu na Rais alishasaini. Je, ni nini kigugumizi cha kushindwa kutenga bajeti ya uanzishaji wa Baraza la Vijana kuanzia Taifa mpaka Kata? Tunahitaji commitment ya Serikali hatutaki ahadi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ester Bulaya, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali kwa agizo hilo la Serikali lililotolewa kupitia Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, tayari imekwisha kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli za vijana katika Halmashauri 84 zimekwisha tenga maeneo kwa ajili ya shughuli hiyo na eneo ambalo ni la mfano katika uzinduzi wa programu hii ya kutengewa maeneo kama agizo la kwenye Halmashauri nchini, lilifanyika hivi karibuni pale Kahama – Zongomela, kuna eneo kubwa ambalo vijana wanafanya shughuli mbalimbali pale zikiwemo pia za kilimo lakini pia biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anauliza ni lini Serikali sasa itaenda katika kukamilisha mchakato wa kupata Baraza la Vijana ikiwa sheria tayari. Tayari eneo hili ni agizo la Mheshimiwa Rais ambaye alizungumza alipokutana na vijana pale Mwanza, alitoa maelekezo na maelekezo hayo yanafanyiwa kazi na kwa kipindi chote tayari tumekwishaanza na mabadiliko kwa sasa. Tumeshafanya mabadiliko ya sera ya vijana ya mwaka 2007 na hatua ya pili itakuwa kwenda katika kuangalia uhitaji wa sasa katika sheria kama italazimika kuweza kufanya mabadiliko.

Mheshimiwa Spika, hatua ya tatu itakuwa sasa kuangalia kulingana na mazingira yaliyopo kama kutakuwa na ulazima kwa wakati wa sasa kuendana na situation iliyopo katika mahitaji ya vyombo vingi pia vya Kimataifa kama tutaweza tukaandaa Baraza la Vijana kwa kipindi hiki, lakini tayari michakato hii tayari tumekwisha kuianza kwa upande wa Serikali. (Makofi)
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri maana yamekuwa safi tofauti na penalty ya Simba ya jana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kwamba hawa watoto wenye walemavu mara nyingi huwa wanarandishwa randishwa mitaani na unaweza ukaja ukamkuta mtoto anarandishwa mtaani na watoto wenziwe maana yake mpaka hawa wengine wanakosa zile haki za watoto.

Sasa ndiyo maana nikauliza ni lini kwa sababu tunaona bado wako mtaani wanarandishwa ni lini hasa hatua stahiki za ukweli ukweli zitachukuliwa ili kupunguza lini wimbi? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili wazee wengi huwa wanashindwa hizo huduma tunazoambiwa wanapewa wanashindwa kuwapelekwa watoto hawa kwenda kupata huduma, wengine wanahitaji kwenda kupelekwa kwenye mashine kufanyishwa mazoezi, lakini wengine wanahitaji mambo tofauti tofauti, lakini ingawa limejibiwa hapa lakini tunaona kwamba ni bado hicho kitu kinaendelea.

Kwa hiyo niiulize Serikali ni lini hili jambo la watoto kupatiwa hizi huduma ambazo wanahitaji wakati mwingine zinatolewa kwa pesa watapata bure ili wale wazee nao waweze kupata faraja? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ali King, la kwanza akiuliza kwamba hawa watoto wamekuwa wakirandishwa randishwa mitaani kwa maana ya kuzururishwa.

Ni lini hatua stahiki zitachukuliwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali wamekwisha kuanza kuchukua hatua hasa pale matendo kama hayo yanapofanyika mitaani na kwa kuzingatia mwongozo huo ambao umetolewa ambao ni Mwongozo wa Taifa Utambuzi wa Mapema Afua Stahiki za Watoto wa Watu Wenye Ulemavu. Lakini pia kwa mujibu wa sheria tulizonazo na moja ya sheria ni hizo za utekelezaji wa sheria za watoto ambapo watoto wana haki na stahili zao zimeainishwa kwa mujibu wa sheria.

Kwa hiyo, pale inapobainika kwamba kuna changamoto kama hizo kwenye mitaa yetu hatua zimekuwa zikichukuliwa kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani kwa sababu zimeainishwa kwa mujibu wa sheria ya mwaka 2019. Kwa hiyo, hatua tayari tumekwisha kuanza kuchukua.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri inatosha ameshakuelewa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu huduma; tayari Serikali imekwisha kutambua watoto zaidi ya 76,247 na ilibaini watoto wenye changamoto hizo ni 42,373 na hivyo tayari umekwisha kuingia kwenye mpango kupitia rejista ambayo iko ya utambuzi chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Makundi Maalum, lakini sambamba na hilo pia Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaendelea na shughuli hiyo ya usimamizi na uratibu wa masuala ya ulinzi na usalama wa Watoto, ahsante.
MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nilikuwa na maswali mawili madogo ya nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani kwa kutumia ofisi zetu za kibalozi kuwasaidia wale vijana wetu wa Kitanzania ambao tayari wameshapata fursa ya kufanyakazi nje ya nchi, lakini mara kwa mara wamekuwa wakipata matatizo na shida ambazo wanakosa kusaidiwa?

Lakini la pili Serikali ina takwimu rasmi za vijana wote ambao wanafanyakazi nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mohamed kwa kuangalia sana haya maslahi ya ajira ya Watanzania nimpongeze sana kwa kazi hiyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ofisi yetu, Ofisi ya Waziri Mkuu inashirikiana vizuri na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje kwa kuhakikisha kwamba masuala haya yanaratibiwa vizuri na hata hivi sasa tumekwisha kuanza utambuzi huo wa vijana wapo ambao walikuwa wanaenda wenyewe bila kutoa taarifa kwenye ubalozi au kwenye nchi na wamekuwa wakipata matatizo mbalimbali tumewaomba na tumetoa rai kwamba waendelee kujisajili kwenye Balozi zetu.

Lakini zaidi ya hapo pia katika mikataba ambayo tumeingia sasa maalum, kwa mfano Qatar tunakuwa na Kombe la Dunia hivi karibuni wafanyakazi wengi tunatarajia kuwapeleka kule na waweze kupata ajira.

Kwa hiyo, haya tunayaratibu vizuri kupitia Wizara ya Mambo ya Nje kwa kushirikiana na balozi zetu huko nchini na hivi karibuni mmeona Balozi wa Ubelgiji alitoa takwimu za maeneo ambayo Watanzania wangeweza kuchangamkia kuweza kupata ajira. Kwa hiyo uratibu upo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu katika maeneo hayo.
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali haioni wakati umefika wa kushirikisha sekta binafsi na taasisi za fedha katika kuwezesha wahitimu wa kilimo kujiajiri kwa uratibu na usimamizi wa Serikali?

Swali la pili; kwa kuwa Benki ya CRDB imeonesha njia ya kushusha riba mpaka asilimia Tisa; je, Serikali haioni kuwa ipo haja sasa kuratibu punguzo hilo la riba, kuweka mpango wa kuwezesha vijana kufaidika na mikopo hiyo kwa ajili ya kilimo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwanza sekta binafsi na taasisi za fedha ambazo zinaweza zikasaidia vijana pengine kuweza kupata nafasi na kuziratibu kwa ajili ya kuwapa nafasi na fursa, hili tunalichukua kama wazo ambalo tunaweza tukawasiliana na Mheshimiwa Mbunge baadae na kuona namna nzuri ya kuliratibu suala hili ili vijana wetu waweze kupata ajira lakini pia kupata fursa mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo ameliulizia kwa mpango mzuri ambao umeanzishwa na Benki ya CRDB wa kushusha riba kwa asilimia Tisa. Nieleze tu kwamba pia katika ofisi ya Waziri Mkuu tayari tumekwishaanza kuchukua hatua mbalimbali ikiwa kuanzia zile fedha zinazotolewa katika ngazi ya Halmashauri asilimia Nne kwa vijana pia fedha ambazo zimekuwa zikitolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana sambamba na hilo na Mabenki mengine ambayo yamekuwa yakitoa riba mbalimbali tunaendelea kuratibu na tayari mazungumzo yamekwishaanza lakini tutamshirikisha Mbunge ilia one hatua hizo na pengine atakuwa na mawazo ya ziada ambayo yatatusaidia zaidi katika kufikia azma njema ya kuwasaidia vijana wetu. Ahsante. (Makofi)
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwa jawabu zuri la Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa baadhi ya wahitimu ambao wanashindwa kupata kazi au kujiajiri wanaamua kuondoka nchini kwenda nchi za nje kufanya kazi na wakati huo mkopo wao huku hawajalipa; ingawa kuna wazazi au wadhamini wanaambiwa wao wausimamie mkopo huo, mzazi huyu ni masikini, hana uwezo wala hajui ataipata wapi hiyo pesa: Je, deni hili hitalipika vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa kuwa baadhi ya wahitimu wako mitaani, hawana kazi, hawawezi kujiajiri na ambao elimu yao ni ya juu; na vile vile wahitimu hao wanapokuwa mitaani wanaweza kufanya mambo ambayo siyo mazuri kisheria, ingawa wao wanasema wanawapa elimu, kuna mkopo wa asilimia 10, wengine wajasiliamali.

Kwa nini wasingewakusanya wakawafundisha kazi za kujitegemea ambazo wazee wetu walikuwa wanafanya, kama upishi wa kitaalam, ufundi wa ujenzi, ufundi mchundo ila ni wa kitaalam kulingana na elimu yao waliyonayo na wakimaliza kuwapatia kitu kidogo ili waweze kujiajiri na kuajiri wenzao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fakharia Shomari Khamis kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwenye eneo la kwanza la wahitimu ambao wanamaliza na kwenda nje ya nchi kufanya kazi na huku wakiacha deni katika bodi yetu ya mkopo, kumekuwa na utaratibu mzuri wa Serikali kwa sasa wa kuendelea kuratibu watu ambao wako nje ya nchi (diaspora) wakiwa wanafanya kazi huko na kuweza kutengeneza arrangement za kuweza kuwafanya wao yale madeni yao yaweze kulipwa. Taarifa hizi tumekuwa tunazipata kutoka upande wa wadhamini wao ambao wanabaki hapa nchini. Kwa hiyo, suala hili tunaendelea kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwemyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa kwa kuliona na kuendelea kuwa mfuatiliaji ili fedha hizi zisipotee ambazo tunatarajia ziwasaidie vijana walio wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ameuliza pia kuhusu wahitimu walio mtaani, kama kuna mpango wowote wa Serikali wa kuwasaidia. Tayari vijana wapo ambao wamechukuliwa na vyuo mbalimbali. Tunavyo Vyuo vya VETA ambavyo vinatoa mafunzo hata sasa. Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan alitoa shilingi bilioni tisa kwa kuwasaidia vijana zaidi ya 14,432 katika Vyuo 72 vya VETA hapa nchini na tayari wanaeleleka kuhitimu katika awamu ya kwanza katika miezi sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kwa sasa ukiangalia katika upande wa Wakala wa Ajira (TaESA) kumekuwa na utaratibu huo wa kuwasaidia vijana kupata ajira na pia kupata mafunzo ya namna ya kuomba kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo, pia tumeingia katika mpango mwingine mpya. Sasa hivi tunafanya study ya kuangalia nchi nyingine ambazo zina changamoto kubwa ya masuala ya ajira na tunafanya study China, Marekani, Uswiss, Ubeligiji, Ufaransa, Rwanda, Burundi na Kenya ili tuweze kuangalia wenzetu kwenye eneo la ajira wamefanya kwa kiwango gani. Hivi karibuni nitatoa taarifa ya kuhusiana na changamoto za ajira jinsi nchi nyingine ambavyo wameendelea kuzikabili. Ahsante.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwa majibu ya Serikali, siku zote yamekuwa yakiamini kwamba tatizo la ajira la vijana litatatuliwa kwa kutegemea Serikali Kuu ama public sector. Sasa ni wazi kwamba Serikali inatoa ajira kwa 2% tu ya mahitaji yote ya ajira. Huo ndiyo ukweli. Mheshimiwa Naibu Waziri ameeleza kwamba changamoto ni private sector ya nchi hii iko duni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limekuwa likielezwa kwenye taarifa zote za Mipango ya Miaka Mitano ya Serikali; 2011, 2015, 2015/2020 kwamba Sekta binafsi ya nchi hii inafanya vibaya. Sasa niiulize Serikali: -

Je, mna mikakati gani na mmekwama wapi mpaka miaka 10 ya Mipango ya Maendeleo ya nchi hii? Mnaonekana mmefeli kabisa kusaidia sekta binafsi ichanue. Kwa sababu ikichanua ndiyo vijana wetu watapata ajira kwenye maeneo mengine. Mmekwama wapi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu la nyongeza la Mheshimiwa Halima Mdee ambaye anauliza tumekwama wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie kwamba Serikali haijakwama popote. Mkakati wa kwanza ambao tumeufanya kama Serikali ni kufanya mapitio yote ya sera katika sekta binafsi ili kuweza kuziboresha zaidi na kuendana na uhitaji wa kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tumechukua hatua pia katika kubadilisha sheria mbalimbali zinazohusiana na masuala ya uwekezaji ikiwemo Sheria ya Kuratibu ajira za wageni ambapo sasa tumebadilisha na kuruhusu watu ambao wanahitaji kuja kuwekeza nchini, kupunguza yale masharti yaliyokuwepo hapo awali; na unaweza ukaona kuanzia hivi sasa hata kufikia yale mapato yanayopatikana kwa kuomba vibali vya kazi, imefikia zaidi ya bilioni 145. Kwa hiyo, hiyo ni hatua kubwa ambayo Serikali Awamu ya Sita inafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo lingine, ipo pia mikakati ya kuandaa maeneo maalum ambayo ni maelekezo katika maeneo ya kuongeza fursa za ajira kwa vijana. Ni agizo la Mheshimiwa Rais kwamba katika kila Wizara ya Kisekta kwenye mwaka wa bajeti itakapotengewa fedha, ile bajeti katika matumizi yake ilete implication ya ajira ngapi zitapatikana kutokana na fedha hizo ambazo zimetolewa katika mwaka wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la nne ni hilo la kimkakati ambao tumeendelea kufanya utafiti katika nchi nyingine. Suala la ajira ni mtambuka na liko ulimwenguni kote. Nitolee mfano China, wana population ya bilioni 1.3, lakini katika population hiyo ya 1.3, tatizo la ajira walikuwa wameli- address kwa asilimia 64 tu. Katika asilimia 40 katika kila mwaka unaoingia kunakuwa kuna immigrants wanaoenda kutafuta ajira kutoka nchi ya China, population zaidi ya watu milioni 150.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna hatua mbalimbali ambazo wamezichukua na tunafurahishwa kwamba ukisoma hizi ripoti na taarifa, hata ile ya International Labor Organization, inaonyesha kwamba Tanzania tumepiga hatua na tumeenda katika mikakati mizuri ya kutatua tatizo la ajira. Ahsante.
MHE. AMINA ALI MZEE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali moja la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, natambua wanufaika wakubwa ni vijana Watanzania: Je, Serikali ina mpango gani wa kupanga fedha kwa ajili ya kukiendeleza chuo hiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBAS P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeshakuwa na mpango wa kujenga jengo hilo litakalokuwa na urefu wa ghorofa sita na tayari fedha zimeshatengwa kwa ajili ya shughuli hiyo. Kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Amina kwa kuwa mfatiliaji.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tuna habari nyingine njema ambayo Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan ameshatoa zaidi ya shilingi bilioni 54 kwa ajili ya kuwasaidia vijana zaidi ya 150,000 ambao wataenda kupata mafunzo mbalimbali katika vitengo hivyo ikiwemo uchumi wa bahari. Ahsante. (Makofi)
MHE. CAPT. ABBAS ALI MWINYI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa chuo hiki kinatoa mafunzo ya aina mbili, yaani nadharia pamoja na practical. Sasa swali ni kwamba, je, Serikali inahakikishaje kwamba kwa wale ambao wanamaliza nadharia na wanatakiwa wafanye practical, hiyo practical inapatikana katika meli gani? Nini mchango mchango wa Serikali katika kuhakikisha kwamba upande wa pili wa practical unapatikana? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBAS P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abbas Mwinyi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ameuliza katika eneo la mafunzo, hasa katika practical training. Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wakala wa TAESA ambaye yuko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tumekuwa tukitoa mafunzo hayo kwa wahitimu, lakini pia kuna mpango maalum wa chuo chenyewe wa utoaji wa mafunzo ya mabaharia ambao wanahitimiu hapo. Kwa mfano ukiangalia takriban zaidi ya vijana 3,000 waliomaliza katika chuo hicho wamepewa mafunzo. Tunatarajia baada ya marekebisho haya na ukarabati wa chuo pamoja na ongezeko la majengo tayari tutakuwa na uwezo wa kudahili vijana 4,500 hadi 6,500 na hawa wote wanaingia kwenye mpango wa mafunzo. Tumekuwa tukiwapeleka kwenye meli za Wakala binafsi au wawekezaji binafsi pamoja na zile za Serikali.

Mheshimiwa Spika, sasa katika ule mpango wa kupata meli yetu wenyewe kwa ajili ya chou, nao utasaidia katika kufanya practical training ili kuwajengea vijana wetu competence na performance katika kazi hii. Ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu. Naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza private sector ni mdau kutoa ajira kwa wananchi ya wananchi wa Tanzania kwa kushirikiana pamoja na Serikali. Tukiangalia katika nyanja mbalimbali private sector imeathirika kwa kiasi fulani especially ukiangalia kwenye mambo ya shule na taasisi nyingine; uendeshwaji wa shule umekuwa ni mgumu kwa kiasi fulani kiasi kwamba utoaji wa ajira kwa vijana wetu umekuwa ni mgumu kwa kiasi kikubwa. Labda kutokana na UVIKO 19 na mambo mengine ambayo yako: Je, Serikali ina mpango gani kusaidia private sector na kufanya tathmini ya kina kwenye private sector kwa lengo la kuisaidia ili iweze kusaidia kutoa ajira kwa vijana wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwenye swali langu la msingi nimesema vijana ambao wamehitimu Vyuo Vikuu zaidi ya 100 wamejiunga pamoja na wapo tayari; na wameweka utaratibu wao, wamesema wenyewe ni kilimo cha makambi; kwamba wanaweza wakakaa sehemu wakaweka kambi, wakafanya kilimo. Walikuwa wanaomba Serikali iweze kuwasaidia mtaji wa pembejeo pamoja na soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza, Serikali ina kauli gani kutokana na hao vijana ambao tayari wameshajitoa, wako tayari kufanya kilimo cha makambi kuweza kuwasaidia ili waweze kupata ajira? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBASS P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, kama ifuatavyo katika maswali yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyooleza kwenye swali la msingi katika swali lake la pili ambapo amesema vijana tutawasaidia vipi ambao tayari wameshaji-mobilize ili waweze kupata fedha au kuwekewa mtaji waweze kuendelea na shughuli zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili kama nilivyolieleza kwenye jibu la msingi ni kwamba tunashirikiana na Wizara ya Kilimo katika kuhakikisha kwanza tunatenga maeneo, na hapo kwenye Jimbo la Mheshimiwa Mbunge tayari kuna ekari 88.9 ambazo zinaweza kuwasaidia hawa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Wizara ya Kilimo itaweka miundombinu na jukumu la mafunzo litabaki kuwa katika Ofisi ya Waziri Mkuu; na tatu, tutaenda sasa katika kuhakikisha mpaka kwenye hatua ya mwisho ya kutafuta masoko kwenye zao la kilimo au zao biashara ambalo watakuwa nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya hapa tuwasiliane, tuweke mpango mzuri kwa ajili ya kuwasaidia hao vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameuliza Serikali ina mpango gani wa kusaidia private sector kwa kuwa ndiyo mdau mkuu pia katika kutoa ajira? Tayari Serikali imeshaanza kuchukua hatua mbalimbali zikiwemo kubadilisha sera mbalimbali hasa zile ambazo zinahusiana na masuala yanayogusa ajira. Katika sera nyingi ambazo ziko katika Wizara za kisekta tumeshaanza kufanya mapitio mapya kuweza kuhakikisha sera hizo zinaendana na usasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, mabadiliko mbalimbali ya sheria ili kuweza kuhakikisha kwamba kunakuwa na uwezekano mkubwa wa private sector kukua kama jinsi ambavyo tumerekebisha sheria ya kuajiri au kuratibu ajira za wageni. Tumeenda pia kwenye mabadiliko ya sheria na sera na mipango ya masuala ya uwekezaji na uchumi. Kwa hiyo, kwenye eneo hilo Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa maelekezo yake, tunaona sasa ameendelea kuweza kuhakikisha kwamba private sector inaweza kufanya kazi kwa ukubwa zaidi na upana ili iweze kuajiri watu wengi zaidi. Nakushukuru.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nina swali dogo la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya ajira kwa vijana yanawekewa msingi na Sera ya Maendeleo ya Vijana ya 2007. Serikali imekuwa katika mchakato wa kufanya mapitio ya Sera ya Maendeleo ya Vijana 2007 kuanzia mwaka 2016 mpaka 2018. Sasa swali ni: Je, Serikali ina mkakati gani wa kukamilisha Mapitio ya Sera ya Maendeleo ya Vijana mwaka 2007 ambayo yameanza kutoka 2016 mpaka 2018 na mpaka leo hajahitimishwa ili mapitio haya yaweze kuratibu ajira kwa vijana na yaweze kuwa na tija zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBASS P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Judith Kapinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameuliza kuhusiana na nil ini Serikali hasa itakamilisha mchakato huu wa sera. Kwanza tunamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake wa masuala ya vijana wakati wote, lakini tayari sisi kwa upande wa Serikali tumeshaenda kwenye hatua mbalimbali; imetoka kwenye hatua ya makundi na wadau mbalimbali kuweza kuwashirikisha ili waweze kutoa michango yao katika sera. Hivi karibuni nadhani kama haitachukua muda sana, ndani ya mwaka huu tutakuwa tumeenda kwenye hatua ya kutoa taarifa rasmi ya namna gani ambavyo tumeenda ukamilishaji wa sera hii ya vijana ya mwaka 2007. Ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru, nadhani kwa majibu haya ya Serikali inanishawishi sasa kuja na Hoja Binafsi Bungeni ili tuwasaidie walimu, tuisaidie pia Serikali na vyama vya wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekiri kabisa kwamba kwa mujibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini kwamba vyama sasa na wanachama wanapanga ada yao ambayo watalipa wanachama.

Sasa nataka kujua; Serikali inapata wapi uhalali wa kukusanya ada za wanachama na kuwapa vyama hali ya kuwa wanajua wako baadhi ya watumishi, hasa walimu wanakatwa bila ridhaa yao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kada ya ualimu ndiyo kada pekee sasa hivi ina vyama vitatu vinavyotetea haki za walimu. Kuna Chama cha Walimu ambacho kinatoza ada asilimia mbili; kuna Chama cha CHAKAMWATA ambacho kinatoza ada asilimia moja; lakini kuna Chama kingine cha KUWAHATA, chenyewe kimeweka fixed amount ya shilingi 5,000.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali haioni haja ya kuleta mwongozo ambao uta-regulate mwenendo wa vyama hivi ili sisi walimu tusiwe soko holela la watu kuja kujitafutia ujira kwenye nanihii yetu hii? Naomba majibu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Sima, amekuwa mtetezi mzuri wa maslahi ya walimu, na yeye mwenyewe amewahi kuwa kiongozi katika vyama hivi vya walimu na kwa hiyo, nimpongeze yeye pamoja na walimu wenzake; Mwalimu Kassim Majaliwa Majaliwa, Mwalimu Jenista Mhagama, Profesa Ndalichako na walimu wengine wengi pamoja na Mwalimu Spika ambaye leo tunaye hapa, Mheshimiwa Dkt. Tulia mwenyewe; nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye jibu, hapa ni kweli kwamba suala hili linasimamiwa kwa mujibu wa sheria na ni Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini ya mwaka 2004. Sheria hii inatoa miongozo wa namna gani ambavyo vyama vya wafanyakazi vinaweza vikasimamia maslahi yake. Na ni takwa la Mkataba wa Kimataifa wa ILO (International Labour Organisation) Sheria Na. 3 katika mkataba huo katika kifungu cha tatu inaeleza kwamba vyama hivi viwe huru na vijiendeshe na kujitaribu vyenyewe, na Serikali anaendelea kuwa regulator tu.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye eneo la vyama kama alivyosema katika zile asilimia, vikao vikuu kwa mujibu wa katiba ndivyo vinakaa na kufanya maamuzi. Lakini hata hivyo, kwenye Chama hiki cha CHAKAMWATA tayari kimekwisha kusimamishwa na msimamizi wa masuala ya vyama vya wafanyakazi na kesi inaendelea, iko mahakamani.

Mheshimiwa Spika, pili, kwenye suala la Chama cha KUWAHATA ambacho wanachaji shilingi 5,000, wanaochajiwa ni wale tu ambao ni wanachama, kama siyo mwanachama hana haki ya kukatwa fedha hizo. Kwa hiyo tutafanya ufuatiliaji na tutashirikiana na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuhakikisha haki za walimu zinalindwa kwa sababu walimu ndio nguzo kuu ambayo inatutengenezea Taifa letu, tunapata wataalam kutokana na walimu na walimu hawa ni wadau wa muhimu kwa Serikali hii ya Mama Samia Suluhu Hassan, na hatutawaacha, tutaendelea kutetea haki zao. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, swali langu la kwanza, je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na wale wastaafu ambao wanapigwa danadana wakati wakifuatilia mafao yao ambayo ni difference au utofauti ya kile kipindi ambacho makato yamepelekwa kwenye mifuko na kile kipindi ambacho hayajapelekwa kwenye mifuko na madai ni kwamba Maafisa Masuuli wamehama au hawakupata uteuzi?

Swali la pili, ningependa kujua kama Serikali itakuwa tayari sasa kuwataka waajiri au kuwahimiza watekeleze masharti ya mifuko haraka iwezekanavyo ili wale wastaafu waweze kulipwa haki zao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kwa kipindi cha nyuma kulikuwa na changamoto ya wazee wetu waliotumikia Taifa kwa nguvu zao lakini pia kwa uadilifu na utumishi uliotukuka, walikuwa wakipata usumbufu katika kupata mafao yao aidha kwa kuambiwa kuleta barua na changamoto nyingine nyingi ambazo zilikuwepo.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako pamoja na mimi na wasaidizi wengine kulikuwa na mpango kabambe wa kuweza kupita katika mikoa yote, kukutana na wastaafu na kutatua changamoto hizo na zoezi hili lilifanikiwa na kwa hatua ya sasa tayari tumekwisha kuanza kutatua changamoto hizo na kama kuna specific case ambayo bado haijafanyiwa kazi, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aweze kutufikishia ili tuchukue hatua haraka sana iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la pili pia kwamba kutokana na waajiri sasa kutokutekeleza wajibu; ni tamko la Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba waajiri wote nchini wanao wajibu wa kisheria kwa mujibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini lakini sambamba na hilo Sheria ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii yaani National Social Security Fund Act ambayo inamtaka mwajiri kuwasilisha michango ya mwajiriwa wake bila usumbufu wowote na wajibu huu upo kwa mwajiri kwa mujibu wa sheria na kama atakiuka, kama jinsi ambavyo tumefanya kwa hawa 123 kuwapeleka mahakamani.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo hata mahakama kwa mujibu wa Bunge lako tukufu lilitunga sheria ambayo mwajiri ambaye atakuwa amekiuka kupeleka michango ya mwajiriwa wake akienda mahakamani anatumia procedure ya summary suit, kwa hiyo hana hata wajibu wa kuweza kujitetea na hatua tunachukua.

Kw ahiyo, niwaombe na kuwataka waajiri wote nchini kutimiza takwa hilo la kisheria ili tusije tukafikishana mahakamani na kuchukuliwa hatua kali zinavyostahili kwa mujibu wa sheria, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, malalamiko haya ni mengi, hebu tusaidie, ni kazi ya nani kuhakikisha mwajiri anapeleka makato anayoyatoa kwenye mshahara wa mfanyakazi na ile anayotakiwa kulipa yeye kuhakikisha inaifikia Mifuko ya HIfadhi ya Jamii; ni kazi ya nani?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa swali zuri; kwa mujibu wa sheria ambayo ilipitishwa na Bunge lako tukufu Sheria ya National Social Security Fund inasema wajibu ni wa mwajiri kufikisha, lakini sambamba na hilo ni wajibu wa mfuko pia kuweza kufanya ufuatiliaji wa michango hiyo kuhakikisha inafikishwa. Kwa hiyo ni pande zote mbili; mwajiri anao huo wajibu kwa mujibu wa sheria lakini mchango wanao ma-compliance officer kwa mujibu wa sehria katika utekelezaji nao NSSF au PSSF au mifuko hii ya hifadhi inapaswa kuendelea kumkumbusha mwajiri na kumpa notice. Na kwa sasa tayari kumekwishachukuliwa utaratibu wa kufungua akaunti ya kimtandao ya moja kwa moja, kila mwanachama sasa anapewa taarifa yake kupitia simu ya kiganjani. Kwa hiyo, kama michango haiendi kwa sasa tunawakamata.

Mheshimiwa Spika, kwa hili kwa kweli tunaendelea na operation kali kuweza kufanya ukaguzi ili kuweza kuhakikisha takwa hili la kisheria linatimia na wastaafu wetu wasisumbuliwe. Ahsante.

SPIKA: Nawaona Waheshimiwa nataka kwenda nalo vizuri, kwa sababu Ofisi za Wabunge zina malalamiko mengi sana ya wastaafu wa nchi hii na tukisema kwamba tutaliacha liendelee mtu anafuatilia mafao miaka miwili anaambiwa michango yako haikuja, kama ni kazi ya mwajiri kupeleka na mfuko unajua mwajiri hajapeleka, ni kazi yao, mfuko umlipe huyu mafao yake wao wakatafute fedha zilipo kwa sababu sio kazi yangu mimi kama mwajiriwa kuanza kusema fedha kama zilikuja ama hazikuja sio kazi yangu halafu huyu mwajiri mimi naweza kumuadhibu asipopeleka? Siwezi. Kwa hiyo, ni kazi ya mifuko kufuatilia fedha ambazo hazijalipwa na ndio maana sheria imeweka isipolipwa kuna riba inayotakiwa kulipwa.

Kwa hiyo, sidhani kama wananchi wanatakiwa kuteseka baada ya kuwa wamelipa kwenye mifuko na mwajiri ameshakata fedha. Ninyi Serikali mtengeneze utaratibu mzuri wa kuisimamia mifuko izitafute hizo fedha iwalipe wastaafu, wasataafu wasiwe wanaseka. (Makofi)

Waziri nakuona umesimama, nadhani tutapata tamko zuri hapo ili wastaafu wetu wawe na utulivu. Ahsante sana karibu Mheshimiwa Waziri wa Nchi.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri kuhusiana na hatua ambazo Serikali inafanya kuhakikisha kwamba wastaafu ambao wamelitumikia Taifa letu kwa uadilifu mkubwa hawapati usumbufu wa kupata mafao.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto ya baadhi ya waajiri kutopeleka michango yao katika mifuko na hivyo kusababisha wasataafu ambao michango haikupelekwa ama kutopata mafao yao kwa wakati au kupata mafao ambayo yana mapunjo.

Mheshimiwa Spika, nilihakikishie Bunge lako tukufu kwamba Serikali imeliona suala hili na tunalifanyia kazi ili kuweza kupata ufumbuzi kwa wale waajiri ambao madeni yao yameshakuwa ya muda mrefu yako ambayo yanafika miaka kumi, bado hajaleta hizo fedha. Kwa hiyo, nilihakikishie Bunge lako kwamba tayari Serikali inafanyia kazi, na niahidi kwamba ndani ya miezi miwili mitatu, tutakuja na muafaka wa kutatua tatizo hili ambalo limekuwa la muda mrefu.
MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita, imeanzisha vyuo vya watu wenye ulemavu, kati ya mafunzo ambayo wanayotoa pale mojawapo ni kutengeneza viatu na hapo hapo katika Wizara hii hii wamefungua kiwanda cha kutengeneza viatu pale magereza Mkoa wa Kilimanjaro; je, katika hiki kiwanda walemavu wameajiriwa na kama wameajiriwa ni wangapi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, kwa kuthibitisha spirit ile ile ya Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji mzuri wa sheria hii ya watu wenye ulemavu, katika kile kiwanda ambacho Mheshimiwa Mbunge amekitaja zoezi bado kwanza kiko katika hatua ya awali ya kuanza kufanya mobilization na ukamilishaji wa ujenzi bado haujatimia.

Mheshimiwa Spika, lakini katika uthibitisho wa hilo kwamba tunazingatia hili kama Serikali, Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kuratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu katika nafasi za walimu 8,000 zilizotoka mwaka 2020 watu wenye ulemavu 242 waliajiriwa ambao ni asilimia 3.2. Sambamba na hiyo katika nafasi za mwaka 2021 za ualimu zilizotolewa zilikuwa nafasi 6,949 watu wenye ulemavu 145 waliajiriwa ambao ni sawa na asilimia mbili.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo pia mwaka 2022 katika usimamizi na utekelezaji mzuri wa Serikali ya Awamu ya Sita, ajira zilizotolewa 9,800 za nafasi ya ualimu watu wenye ulemavu 261 walipata sawa na asilimia
2.66. Katika sekta ya afya na maeneo mengi sababu ya muda nafasi 7,612 ambazo zilitolewa watu wenye ulemavu waliopata nafasi hiyo ni 0.63 kulingana na sifa na vigezo ambavyo viliwekwa.

Mheshimiwa Spika, katika Serikali hii tumeweka minimum standard, kwamba hata vile viwango vya ufaulu tunaviangalia katika hali ambayo yule anakuwa sifa kwa sababu watu wenye ulemavu wanakuwa wachache katika uombaji wa nafasi hii.

Kwa hiyo, tutaendelea kuzingatia sheria na kuhakikisha kwenye private sector na Serikali tunazingatia takwa hili la kisheria la kuajiri watu wenye ulemavu, kwa sababu kufanya hivyo pia ni ibada kwa nchi.
MHE. HUSNA J. SHEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijana hawa ambao ni mafundi, wamekuwa wakikosa kazi kwenye maeneo tofauti tofauti kwa kigezo cha kukosa cheti, na wale ambao wana vyeti wamekuwa wakichukua hizi kazi na kuwa kama madalali, kazi hizi zinakuwa zinatekelezwa na hawa ambao hawana vyeti.

Je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kurasimisha kwa kuwapa vyeti hawa mafundi ujenzi, mafundi seremala, mafundi cherehani ili waweze kuajiriwa katika maeneo mbalimbali?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, pale Lukozi, Wilaya ya Lushoto kuna vijana ambao wanatengeneza maji ya betri kwa ajili ya magari na pikipiki. Lakini jambo hili limezungumzwa mara kadhaa ndani ya Bunge hili lakini bado vijana wale hawajapatiwa namna ya kurasimishwa na kutambulika kama kibaji kipya katika Taifa letu.

Je, Naibu Waziri yupo tayari sasa kutembelea vijana wale na kuwarasimisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PATROBAS P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Husna kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika utoaji wa mafunzo haya ya urasimishaji ujuzi, unaenda sambamba na utoaji wa vyeti pia vya mafunzo ili waweze kutambulika na zaidi ya hapo Serikali ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan, tunaenda hatua mbali zaidi hao vijana wanaomaliza vyuo vikuu na kurasimishiwa ujuzi, mbali na kuwapa vyeti, tunawakutanisha na halmashauri ili waweze kupewa fedha kwa ajili ya kuanza kama start-up capital katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwapeleka maeneo ya practical placement kwa maana ya sehemu ambazo wanaweza wakajifunza kufanya kazi, lakini pia kuajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaenda sambamba kwa sehemu kubwa zaidi ya 1,800 wamekwishakupata kazi kwa fedha zilizotolewa mwaka jana wa fedha shilingi bilioni tisa na Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, nakubaliana naye kwamba nitawatembelea vijana hao na hata wengine walioko nchini kama wana ujuzi na maarifa makubwa kama hayo wanayoyafanya, Ofisi ya Waziri Mkuu iko wazi muda wote kuweza kuwahudumia, tuendelee kupata taarifa lakini tunaendelea kuwatambua na kuwahudumia, lakini kuweza kuhakikisha tunawasaidia. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa madereva wengi wamekuwa wakifanya kazi na kupata ajali lakini na matatizo mengine ya kiafya hali ambayo wanakuwa mzigo kwa familia. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia hawa madereva waweze kupata haki zao za msingi kuepukana na vifo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tamko limetolewa muda mrefu na mpaka sasa kuna baadhi ya wamiliki wa magari hayo hawajatoa mikataba hiyo. Je, nini tamko la Serikali kuhusiana na hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza Mheshimiwa Kisangi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, madereva ambao wanaopata ajali au maafa kutokana na kazi ambazo wanazifanya, Serikali imeweka utaratibu mzuri wa kuanzisha Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) ambao unawajibika na kuhakikisha kwanza maeneo yote rasmi ya waajiri yanasajiliwa na kutoa michango kwa ajili ya fidia pale mfanyakazi anapopata madhila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo Sheria ya Workers Compensation ambayo nayo pia inahusika na masuala ya ulipaji fidia. Sambamba na hilo Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, amefanya mabadiliko na maboresho kwenye sheria za bima ambapo vyombo hivi vinakatiwa bima na zipo bima ambazo zinawa-cover pia wale ambao watapata madhila kutokana na ajali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la nyongeza la Mheshimiwa Kisangi ameuliza kuhusu waajiri ambao hawajatoa mikataba. Naomba nitoe tamko rasmi la Serikali kama jinsi alivyonitaka nifanye, tamko rasmi ni kwamba, ni kosa kisheria kama umeajiri mfanyakazi na haumpatii mkataba, kwa sababu sheria zinatoa maelekezo, Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, inatoa haki za mfanyakazi, lakini pia wajibu wa mwajiri. Wajibu wa mwajiri unaelezwa katika sheria hiyo zikiwa ndiyo haki za mfanyakazi. Kwa hiyo, ina reciprocate kwamba haki za mwajiri, ndio wajibu wa mfanyakazi na wajibu wa mfanyakazi ndio haki za mwajiri. Kwa hiyo, mtu yoyote ambaye hatatoa mkataba wa kazi na maeneo hayo tumekuwa tukiyabaini, tumekuwa tukiwachukulia hatua na ikibidi kuwapeleka mahakamani ili waweze kutekeleza hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe rai kwa maeneo yote Watanzania wanaonisikiliza lakini pia Waheshimiwa Wabunge, kama kuna maeneo ambayo tuna uhakika kwamba hawatoi mikataba ya kazi pamoja na kaguzi zetu mtupe taarifa ili tukachukue hatua stahiki kwa wakati unaostahili. Ahsante.
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, kwanini Serikali isiridhie sehemu ya mkataba huo ambayo haina matatizo wala ukakasi ili kuwasaidia wafanyakazi wa majumbani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Serikali inawasaidaje wafanyakazi wa private sectors wakiwemo wa mahoteli na kwenye baa waweze kujiunga na vyama vya wafanyakazi ili kulinda maslahi yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Thea Medard Ntara, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba mambo ambayo hayana madhara yanayoendana na mila, tamaduni na desturi ya nchi yetu, tayari sheria yetu ya ajira na mahusiano kazini ya sura namba 366 imeshayazingatia hayo na tumeyafanyia domestication kwa maana ya kuchukua na kuyaweka kwenye sheria zetu za ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika eneo hilo, siyo mikataba yote ya Kimataifa ambayo tunairidhia kwa ujumla wake. Tuna haki kwa mujibu wa Sheria za Kimataifa ya kusaini tu, lakini kuna process nyingine ya kufanya ratification na baada ya hapo unaweza ukawa unafanya reservation. Kwa hiyo, tuna reservation kwenye baadhi ya vifungu vya Mkataba huu wa Kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hilo, nimhakikishie Mheshimiwa tayari Serikali ina utaratibu mzuri wa kuhusiana na Mikataba ya Kimataifa kwenye masuala ya haki za wafanyakazi kwa mujibu wa Shirika la Kazi Duniani (International Labour Organization). Sambamba na hilo, tunaendelea kuratibu hata wale wafanyakazi wa majumbani walio nje nchi, kwa mfano, kwa nchi za Mashariki ya Kati, kule Oman, wako zaidi ya wafanyakazi 14,000 ambao walikuwa wanafanya kazi kule na 55 wako kwenye kada nyingine tofauti na ufanyakazi wa majumbani.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri, umejibu vizuri hilo swali, tuendelee.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili la kuhusiana na wafanyakazi wa hotelini kuingia kwenye vyama vya wafanyakazi, tunayo pia sheria inayohusiana na masuala ya Trade Unions ambayo ni sheria inayoratibu uwepo wa Trade Unions. Vyama hivi vya wafanyakazi wana haki ya kukusanya wanachama katika maeneo mbalimbali yaliyosajiliwa. Kwa hiyo, tayari utaratibu huo unafanyika na tumeshaanza kutembelea baadhi ya hoteli na maeneo mengine kuhakikisha wafanyakazi hawa wanapewa mikataba na kulinda haki zao za msingi. Ahsante.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu aliyoyatoa Naibu Waziri, ukitazama Viti Maalum vina utaratibu maalum ambao umeshushwa na Tume mpaka kwenye vyama vya siasa. Je, haiwezekani sasa kuhakikisha kwamba utaratibu huu unashushwa ndani ya vyama vya siasa ili vyama hivi viwajibike kuwateua wazee ili na wenyewe waweze kupata nafasi ndani ya Bunge?

SPIKA: Mheshimiwa Conchester Rwamlaza hebu tusaidie, hilo kundi la wazee, unataka kundi la wazee kwa ujumla au kundi la wazee wanawake?

MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, kundi la wazee kwa ujumla wao bila kujali wanawake au wanaume.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PATROBAS P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Katiba yetu imeainisha vizuri katika vifungu hivyo, lakini pia ipo katika kifungu cha 36, 37 na 61 ambavyo vinatoa haki ya uwakilishi, lakini pia Ibara ya 21 ya Katiba, nayo pia inatoa haki ya kushiriki kwenye majukumu moja kwa moja ama kupitia uwakilishi. Zaidi kwenye Ibara ya 3 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaeleza Tanzania ni Nchi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi ya kidemokrasia, kijamaa isiyofungamana na dini au isiyofuata misingi ya dini na ina mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Mheshimiwa Spika, sasa katika vyama vingi vya siasa kwa mujibu wa sheria ya mwaka 1992, vyama vya siasa vinapewa haki ya kupata wawakilishi kwenye vyombo mbalimbali vya maamuzi, ikiwemo vyama hivi vya upinzani. Kwa mfano mzuri tu ambapo moja ya chama ambacho kinafanya hapa nchini vizuri kuna jumuiya ya vyama ambazo zinakuwa na wawakilishi wake, kuna moja ya chama kina umoja wa vijana UVCCM, lakini pili chama hicho kinao umoja wa wanawake, lakini pia kuna umoja wa wazazi na wawakilishi hao wote wameendelea kuwemo humo.

Mheshimiwa Spika, pengine hata Mheshimiwa naye atanikubalia, naye ni mmoja wa wawakilishi katika chama chake kwa sababu ni bibi yangu na ni mama, Mheshimiwa Conchester, kwa hiyo, nafasi hiyo inatolewa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kufuatia majibu mazuri ya Serikali lakini bado changamoto inayoyakuta makundi haya ni pale unapokwenda kwenye taasisi za kifedha na kushindwa kufungua akaunti ya mtu mmoja. (Makofi)

Sasa ni lini Serikali itafanya makubaliano na mabenki ili makundi haya yaweze kunufaika na mikopo hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kufuatia hali ya watu wenye ulemavu na mazingira magumu ya biashara, je, Serikali haioni haja ya kuongezea muda marejesho makundi haya ikawa tofauti na makundi ya kinamama na vijana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Janeth kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza naomba tulichukue kama ushauri na nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji huo kwamba tutaona namna bora ya kuwasaidi watu wetu katika kuona utaratibu wa kupata mikopo kupitia taasisi hizo kama alivyoshauri.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, la kuhusiana na muda wa marejesho ni kweli tumekwishakuliona hilo Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba watu wenye ulemavu ni kweli kwamba wanachangamoto. Unaweza ukakuta mtu wa kawaida ni tofauti na mtu mwenye ulemavu kwa sababu kuna wakati anahitaji kuwa na msaidizi ambaye yeye amekopa sawa, kama ni milioni 10 na mtu ambaye ni mzima naye ana milioni 10 lakini akienda kununua bidhaa atajikuta anahitaji kwenda na mtu wa kumsaidia kuona hizo bidhaa au kumsaidia kwenye usafiri.

Mheshimiwa Spika, pili hata atakapopata hitaji la chakula atahitaji amnunulie tena chakula msaidizi wake, na tatu hata anapokuwa anafanya biashara yake kwenye yale mazingira kama ni ana ulemavu wa kutokuona, atalazimika awe na mtu pale. Kwa hiyo, gharama inakuwa kubwa tofauti na hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeliona hilo na tunaona sasa namna gani ambavyo tunaweza tukaona utaratibu wa kubadilisha kanuni ili kuweza kuwanufaisha zaidi watu wenye ulemavu kwa sababu kama unavyofahamu hujafa hujauumbika sisi wote ni watarajiwa kwa matakwa ya Mwenyezi Mungu, ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa gharama za maisha kwa wananchi wote bila kujali kama wanafanya kazi sekta binafsi au sekta za umma ni zilezile gharama kama mchele, unga na gharama nyingine.

Je, Serikali ina mpango gani ya kuhakikisha kwamba mishahara kwenye sekta binafsi na yenyewe inapanda inakuwa angalau shilingi 370,000 kama ilivyo kwa sekta ya umma? Kwa sababu sasa hivi maeneo mengi ni shilingi 100,000 kuendelea kidogo.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, amesema kwamba wanategemea kutoa mwongozo wa kupandisha mishahara kwa sekta binafsi mwezi Novemba; je, watakapotoa miongozo na mishahara itakapopanda, wakati wengine wa Serikali tayari wameshapandishiwa mishahara toka tarehe 1 Julai; je, mwongozo huo pia utalipa na malimbikizo kwa muda ambao wenzao wameshaanza kulipwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu la nyongeza la Mbunge wa Arusha, Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza niseme tu kwamba katika mishahara hii ya watumishi wa umma na wale wa sekta binafsi kuna utofauti mkubwa. Katika sekta binafsi tunazo kada tofauti tofauti, wapo wafanyakazi wa mashambani, wapo wa viwandani, wapo ambao ni makampuni binafsi, wapo waliojiajiri wenyewe na ambao wameweza kuajiri watu wachache. Kwa hiyo, uki- standardize na ukawa na standard level ya mishahara kwa kima cha chini inaweza ikaleta ugumu sana tumefanya study kuna best practice katika nchi nyingi ambazo tumeona kwamba huwezi uka-standardize kila mmoja na ndiyo maana bodi inaundwa ili ikafanye utafiti katika kuangalia uhalisia wa hali ya uchumi, lakini pia kazi zinazofanyika katika kila eneo ili iweze kuweza kupanga kulingana na category walizonazo hao wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wafanyakazi wa viwandani wana category yao, lakini pia na wale wa mashambani na maeneo mengine kulingana na uhalisia wa uchumi wa nchi husika. Kwa hiyo, tumelifanya hilo utafiti katika best practice ya nchi zaidi ya saba Mheshimiwa Mbunge. Kwa hiyo, niña imani kwamba bodi ya kima chini italeta ushauri ambao ni sahihi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, ndiyo mwenye dhamana ya kuamua kwamba hapo kuna haki? Kwa sababu tunachopaswa kuangalia ni zile kazi za staha lakini atumishi aweze kulipwa mshahara wake ambao unafanana na hali halisia ya uchumi.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ameuliza kuhusu mishahara hii kwamba kwa upande wa Serikali tayari tumeshatangaza mabadiliko ya mishahara. Kwa upande wa private sector kama kutakuwa na malimbikizo.

Mheshimiwa Spika, kwa nchi yetu hatuna utaratibu wa restrospectivity, tuna utaratibu wa pale sheria au agizo linapotolewa ama kanuni, itakapopitishwa ndipo kwenda mbele hatua hiyo inafanyika. Kwa hiyo, hili suala la mishahara litaanzia pale kima cha chini kitakapokuwa kimerasimishwa na kutangazwa na Serikali. Ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsanta, nashukuru kwa majibu mazuri, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Kutokana na upungufu wa vifaa vya makuzi kwa watoto njiti kwenye hospitali zetu; njia kubwa inayotumika kulelea watoto ni kwa kukubambatiwa na mama zao yaani kangaroo style.

Je, Serikali haioni kuchelewesha marekebisho ya sheria kunaendelea kuhatarisha afya na uhai wa watoto hao? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, watoto njiti wana haki ya kuishi na kulelewa katika mazingira mazuri kama watoto wengine.

Je, Serikali haina timeframe ya kufanyia marekebisho ili kuhakikisha kwamba uhai wa watoto hao unalindwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Judith Kapinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imekwishakuanza kuchukua hatua mbalimbali za kufanya maboresho katika sekta ya afya ikiwemo pamoja na ununuzi wa vifaa ambavyo vinawasaidia watoto hawa kuweza kukua.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, katika eneo hilo hilo, maboresho yamekuwa yanafanyika na Serikali imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali ipo moja ya taasisi katika taasisi nyingi ambazo zinafanya na Serikali, Doris Mollel Foundation pamoja na Vodacom wamekuwa wakifanya kazi hii kwa kushirikiana na Serikali na maeneo mengi tumeona wamefanya kazi kubwa ya kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuhusu haki ya watoto, tayari Serikali kwa kuona umuhimu wa watoto lakini pia generation tayari ilikwishatunga sheria ya mwaka 2009 sheria ya mtoto ambao inatoa haki, moja ya haki ya msingi ambayo iko kwenye Katiba, haki ya kuishi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika kufanya hivyo Serikali imeendelea kuboresha katika sekta ya afya na kuweza kuhakikisha kwamba katika mazingira haya hata mabadiliko ambayo yanatakiwa kufanyika kwa upande wa Serikali tunayachukua haraka sana na kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, niseme tu katika hatua ya awali, tulikwishakuwinda Dar es Salaam, na tukakutana na taasisi mbalimbali/Asasi za Kiraia ambazo zilikuwa na ajenda hii hii na nilikuwa mgeni rasmi katika shughuli hiyo ya kuweza kuona namna gani tunaweza tukachukua best practice katika nchi yetu kuweza kuona tunawasaidia mama hawa wanaojifungua watoto njiti na kupunguza vifo. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru na kuipongeza Serikali kwa majibu yake mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa maeneo ambayo Kamati hizi zimekwishaundwa hazifanyi kazi kwa mujibu wa Sheria Na.9 ya Mwaka 2010. Je, ni sababu zipi zinazosababisha Kamati hizi kutokufanya kazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; naipongeza pia Serikali kwa mikakati mizuri ambayo imewekwa kwa ajili ya ukamilishwaji wa kuundwa kwa Kamati hizi. Kutokana na umuhimu wa Kamati hizi na hasa ikizingatiwa kwamba zoezi hili limechukua muda mrefu kukamilika, je, ni lini Kamati hizi zitakamilika kuundwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya maeneo ambapo Kamati hizi pamoja na kuundwa hazijawa na utekelezaji mzuri wa ufanyaji kazi. Changamoto hii siyo ya kisheria zaidi, sheria imeelekeza ziundwe na tayari zimekwishaundwa, changamoto iko katika eneo la kwanza ni elimu kwa wahusika wenyewe walio kwenye Kamati, lakini sehemu kubwa ni uwajibikaji wa wale ambao wamechaguliwa kuzihudumia Kamati hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni usimamizi wa Kamati zenyewe. Jambo hili naomba nitumie Bunge lako Tukufu kwa niaba ya Waziri Mkuu kuwaomba na kuwaelekeza pia Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala, pamoja na Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya na Makatibu Tawala wa Wilaya waweze kusaidia na kusimamia utekelezaji wa sheria hii ili kuweza kuhakikisha inaleta ufanisi kama jinsi ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la nyongeza ameuliza kuhusu utekelezaji, kwamba lini tutakuwa tumekamilisha zoezi hili. Nieleze tu kwamba Serikali tunaendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu kuweza kuhakikisha Kamati hizi zinafanya kazi effectively na wale ambao hawajaunda kupitia Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wahakikishe kwamba Kamati hizo zinaundwa na ufanisi upatikane.

Mheshimiwa Naibu Spika, itambulike kwamba suala la kutekeleza Sheria Na.9 ya Mwaka 2010 ya Watu Wenye Ulemavu sio suala la hiari, ni suala kisheria na ni la haki za binadamu.
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Ahsante kwa majibu yako Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mchakato wa Mkataba Na. 189 umefikia wapi ili kuboresha mishahara ya wafanyakazi wa majumbani?

Swali langu la pili, suala la kuboresha mishahara ya Wakuu wa Vyuo Vikuu limefikia wapi mpaka sasa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Thea Medard Ntara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari kuhusiana na Mkataba wa Kimataifa Na. 189 tunafahamu kwamba Serikali yetu tayari ilikwisha kuanza kufanyiakazi kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na kulikuwa kuna vipengele ambavyo bado tulikuwa tunaendelea kuvifanyia kazi kwa maana ya kwamba, vipo ambavyo vinavyoendana na hali yetu ya kiuchumi na uhalisia wa kimazingira pamoja na tamaduni zetu, lakini kuna vifungu vingine ambavyo vilionekana na katika msingi wa Sheria za Kimataifa kuna kusaini Mkataba wa Kimataifa, unaweza uka - ratify lakini pia ukawa una- reservation kwenye baadhi ya maeneo. Kwa hiyo, hizo hatua zote Serikali inaendelea kuzichukua kwa haraka, nina imani ndani ya kipindi cha mwaka huu wa fedha hayo yote tutakuwa tumekwisha kuyaangalia hasa kuhusiana na haki na stahiki za mikataba ya wafanyakazi wa ndani.

Mheshimiwa Spika, katika hilo tumeanza awali kupitia Kamishna wa Kazi kuweza kuona namna gani ambavyo tunaweza kutengeneza standard ambazo zinaendana na nchi yetu za kuangalia maslahi kwenye kundi hili ambalo kimsingi maeneo mengi wanakuwa na uonevu na manyanyaso mengi. Kwa hiyo, tunaliangalia sana kama Serikali.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Medard Ntara ni kuhusu maboresho ya mishahara katika Vyuo Vikuu. Hili tayari limeanza kufanyiwa kazi na Ofisi ya Waziri Mkuu ambaye ni mratibu na Wizara ya Elimu ambayo pia ndiyo yenye dhamana hii katika kuangalia. Tunazidi kuangalia viwango kulingana na hali ya kiuchumi, pia uhalisia wa kidunia kwa sasa. Kwa hiyo, hivi karibuni Mheshimiwa Ntara nitamueleza hatua ambazo tumekwisha kuzifikia. Kwa hatua ya sasa siyo vema sana kuzitaja hapa hadharani. Ahsante. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, kwa kuwa suala hili limekuwa likijitokeza mara kwa mara. Je, Naibu Waziri atakuwa tayari kuambatana na mimi kwenda kukutana na wafanyakazi hawa ambao wana malalamiko ya muda mrefu ili kuweza kuwapatia majibu waweze kufunga shauri hili mara moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kama nilivyoeleza na kujibu kwenye swali la msingi kwamba sisi tuko tayari kuweza kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Mheshimiwa Mbunge ili kwenda kutatua changamoto za wafanyakazi hawa na kuweza kulifanyia uchunguzi wa kina, kama wapo wanaostahili kulipwa basi watalipwa na tutaweza kilifanyia kazi.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kiwanda cha Nyuzi pia Tabora kina matatizo kama ambayo yapo kule Ukonga. Wafanyakazi waliachishwa muda mrefu lakini wengi hawakupata mafao yao. Nilikuomba Mheshimiwa Waziri kama utakuwa tayari tuambatane ukawa umeniahuidi lakini mpaka leo naona bado sijui lini utakuwa tayari ili ukawasikilize wale wafanyakazi, kwa kweli hali zao ni mbaya sana, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka ambaye kimsingi ameeleza pia hali ya changamoto zilizo katika viwanda vilivyokuwa kama Kilitex pamoja na Sunguratex, hali hiyo ipo pia kwenye Kiwanda cha Nyuzi kule Tabora. Mimi nipo tayari kuweza kushirikiana naye hata kuambatana nae ili kuweza kutatua changamoto hiyo lakini katika hatua ya awali pia tutapata nyaraka na idadi ya majina hayo ili tuweze kuona urahisi zaidi wa kuwahudumia wananchi wetu, ahsante. (Makofi)
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina swali moja la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo vya ubakaji na ulawiti kwa watoto vimekuwa vikiongezeka siku baada ya siku, na utaratibu wa kuendesha mashtaka ya kesi za ubakaji na ulawiti kwa watoto kulingana na Sheria ya Ushahidi (Evidence Act) inampa mtoto mzigo wa kuthibitisha kwamba amebakwa ama amelawitiwa.

Sasa Serikali haioni umuhimu wa kufanyia mapitio Sheria ya Ushahidi ili kuhakikisha mazingira ya kutoa ushahidi katika kesi za ubakaji za watoto pamoja na kesi za ulawiti kwa watoto zinawekewa mazingira zinazolinda haki za Watoto katika kesi hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu swali la Mheshimiwa Judith Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum, kama alivyouliza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba matendo ya ulawiti kwa watoto na ubakaji yamekuwa yakikithiri, lakini halitokani na mapungufu kwenye sheria.

Moja, sheria kwenye makosa ya jinai, uthibitisho au threshold ya kiwango cha uthibitishaji wa makosa ya jinai ni beyond reasonable doubt yaani uthibitishe pasipo kuacha shaka yoyote na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuliona hili na akaunda Tume Maalum ya Haki Jinai ambayo jana ilifanya kazi hiyo, ikiwa mojawapo ni kuhakikisha kwanza vyombo vyetu ambavyo ni functionalize of the law ambapo ni Ofisi ya Mwendesha Mashtaka, Polisi ambao ndio wanawajibu kwanza wa kupokea ripoti ya uhalifu wa utendekaji wa kosa, lakini pili kufanya uchunguzi; na tatu kupeleka sasa kupitia Ofisi ya Solicitor General kupeleka mashtaka mahakamani; na nne kazi ya mahakama kwa maana ya dispensational of justice.

Sasa changamoto ya mambo haya na ukizungumzia na Sheria ya Ushahidi alivyoieleza Mheshimiwa iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2004, sheria hii inaeleza kiwango cha uthibitishaji ni pasipokuacha shaka, kwa sababu ukiacha hivyo athari yake kuna watu wanaweza wakaumizwa kwa sababu ya kesi za kutengeneza. Ushahidi umeonekana unaharibika kwanza katika ngazi ya upelelezi, watoto wanafanyiwa matendo haya na wakati mwingine kunakuwa hakuna ushahidi kwa mfano ujazaji wa PF3, na kesi inavyoenda kule inakuwa imeharibika, lakini eneo lingine la uharibifu wa mashauri haya na kushindwa kuthibitisha ni pale ambapo waendesha mashtaka au wale wazazi kunapokuwa na dhamana, yule mtuhumiwa anatoka nje na anaharibu ushahidi. Wapo ambao ushahidi unaeleza wamekuwa waki bargain na wazazi na wanalipana huko na matokeo yake haendi mahakamani kwenda kutoa ushahidi na mahakamani huwezi ukashinda kesi bila kuwa na ushahidi.

Mheshimiwa mwenyekiti, pili; inatokea katika mazingira ambayo sheria zetu katika usimamizi wake ile enforcement katika dispensational of justice namna ya utoaji wa ushahidi kwa watoto wadogo, nimkumbushe tu Mheshimiwa Judith Kapinga kwamba Sheria ya Ushahidi inatoa usikilizaji wa mashauri haya in camera, kwamba hayasikilizwi kwenye public hearing kwa maana ya aibu na kutunza ile heshima ya mtoto. Kwa hiyo, wale wasaidizi wake wanaweza wakamsikiliza na bado Sheria hiyo ya Ushahidi inatoa haki pia ya kupima uwezo wa mtoto kama ana uwezo wa kutoa ushahidi mahakamani au mtu mwingine aweze kusimamia hilo.

Kwa hiyo, kwenye eneo la Sheria ya Ushahidi bado tutaweza kuona kama kuna mapendekezo ambayo anayaona, nishukuru tu kwamba ameweza kuliona tutayachukua na kuweza kushauriana na mamlaka kuweza kuona maeneo gani ambayo tunafikiri sheria ina mapungufu na kwa kufanya tu hilo hata Wizara ya Maendeleo ya Jamii tayari wamekwishakaa kikao na kuona kama tunaweza tukaondoa dhamana kwenye makosa ya aina hii, ahsante.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

(a) Kwa kuwa vitendo vya kikatili vya kupiga wanafunzi vimekuwa vingi katika shule. Je, Wizara ya Elimu italiambia nini Bunge hili, usalama wa wanafunzi wanapokuwa shuleni?

(b) Kwa kuwa, walimu wanaofanya vitendo hivyo, wanaangaliwa wanapokuwa wanakwenda shuleni kwamba hawana viashiria vya ulevi hata wakafanya vitendo vya kikatili vya namna hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamis, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye suala la Walimu na matendo yanayokithiri ya kupiga wanafunzi tayari Wizara ya Elimu imekwisha kuanza kuchukua hatua mahsusi za kufanya ufatiliaji kwenye maeneo yote ambayo tumekuwa tukipata taarifa kwamba wanafunzi wanatendewa visivyo, kinyume na utaratibu wa kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo katika hatua nyingine kupitia Wizara yetu Ofisi ya Waziri Mkuu, tunaweza tukashirikiana vizuri na Wizara ya Elimu ili kuweza kubaini kama matendo hayo ya wale watuhumiwa ambao wanaonekana wametenda matendo ya ukatili kwa watoto, kama itaonekana kwamba wana viashiria vya ulevi basi tutachukua hatua kuweza kuhakikisha kwamba masuala haya hayajitokezi tena katika nchi yetu na kuchukua hatua zinazostahili. (Makofi)
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Moja; Serikali ina makakati gani wa dharura wa kudhibiti biashara holela, uingiaji wa mikataba mibovu na usimamizi hafifu wa sheria ambazo kasoro hizo zinasababisha ajira nyingi za Watanzania kupotea?

Mbili; kwa nini Serikali isiachane na utaratibu wa sasa hivi wa baadhi ya ajira kupatikana kwa njia ya uteuzi na badala yake ajira zote zikapatikana kwa njia ya ushindani, ajira za Viongozi na ajira za Watendaji, Mawaziri, Wakurugenzi na Makatibu Wakuu na Watendaji wengine wote wa Serikali ili kuiwezesha Serikali kupata Viongozi wenye uwezo usiotiliwa mashaka katika nafasi mbalimbali za Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, Mbunge wa Kisesa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ameeleza ni mkakati gani ambao Serikali imeendelea kuchukua kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hakuna mikataba mobovu pia utumiaji mzuri wa fedha ambazo zinaenda kwenye maeneo ya uwekezaji ili kuweza kulinda ajira za Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayofuraha kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba tayari Serikali kupitia vyombo vyake muhimu imekwisha kuanza kuchukua hatua na mtakumbuka Mheshimiwa Rais katika nyakati zote amekuwa akichukua hatua katika kuimarisha vyombo vyetu vinavyosimamia sheria, ikiwemo Mahakama lakini pia Polisi, TAKUKURU kwa maana ya PCCB (Prevention and Combating Corruption Bureau) ambayo inapambana na maswala ya rushwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine Serikali imeendelea kuweza kuchukua hatua kwa wale ambao wamekuwa wakiingiza katika mikataba mobovu, hatua mbalimbali zimekwisha kuchukuliwa na Serikali tayari ina Mahakama maalum kuchukua hatua kwenye masuala ya rushwa. Kwa mfano, tunayo Mahakama ambayo inasimamia masuala ya makosa ya kiuchumi, ambayo hii mojawapo ni kudhibiti haya ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake pili ameeleza kwamba ajira kwa nini zisipatikane kwa njia ya ushindani badala ya uteuzi jinsi ilivyo. Kwa sasa, Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inaeleza namna na mfumo wa uendeshaji wa Serikali na inatambua uwepo wa ajira ambazo zinapatikana kwa utaratibu ambao Mheshimiwa Mbunge ameusema wa ushindani lakini pia zipo ajira zinazopatikana kwa njia ya uteuzi kulingana na provisions zilizopo katika Katiba, zipo pia ajira ambazo zinapatikana kwa utaratibu wa kuomba ama kuzipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo katika kupanua wigo wa ajira, Serikali imekwisha kuchukua mikakati ya kuhakikisha tunatafuta ajira ndani na nje ya nchi. (Makofi)
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika formula ya kikokotoo kilichopita watumishi wengi walikwishakopa na wanaostafu sasa hivi walikwishakopa sana.

Je, Serikali ilishaliona hili jambo kwamba hatma yao ni nini, kwa sababu kikokotoo cha sasa kimekuja na formula nyingine ambayo wanatoka kana kwamba mafao yao ni zaidi ya nusu hawajapata?

Je, Serikali ilishafikiria jambo hili na nini hatima ya Watumishi hawa ambao mafao yao yalishaiva na walishakopa kupitia formula iliyopita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, kabla ya kufanya uamuzi huo, mchakato huu ulishirikisha wadau wote na kuliandaliwa actuarial report. Katika kufanya hivyo tulibaini mambo kama hayo ambayo Mheshimiwa Mbunge amesema na nimpongeze sana kwa kuendelea kuwa mfuatiliaji mzuri.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali wakati wa kufanya hivyo, kikokotoo kipya kimesaidia kuja kuongeza lile pato la kila mwezi. Ni tofauti hata na kikokotoo kile cha awali ambacho hakikuweza kuleta tija zaidi.

Kwa hiyo, mengine kwa sababu ndio tumekwisha anza na sheria zetu zimekwisha anza, hakuna ule msingi wa retrospectivity kwa maana ya sheria kuanza kufanya kazi kwenda mbele na sio kurudi nyuma. Tutazidi kuyazingatia yote hayo na changamoto ndogo ndogo zinazojitokeza ili kuweza kuhakikisha jambo hili linaleta maslahi makubwa kwa wafanyakazi na tija, kwa sababu Serikali inaheshimu sana nguvu kazi ya Taifa ambayo ndiyo inaweza kuleta maendeleo endelevu kwa ajili ya taifa letu, ahsante sana.
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza na nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; mfuko huu upo chini ya ofisi ya Waziri Mkuu, Serikali haioni haja sasa ya kuendelea kutoa fedha hizo kwa vijana wa Tanzania Bara na Tanzania Visiwani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, mbali na mikopo kuna fursa nyingine zipi zinaweza kupatikana katika Ofisi ya Waziri Mkuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Latifa Khamis Juwakali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi la awali, suala hili linaongozwa kwa mujibu wa sheria ya fedha ambayo ni Sheria Namba 6 mwaka 2001, kwa masuala ambayo hayahusiana na Muungano. Lakini kwa kuwa tuna mashirikiano mazuri na upande wa Tanzania Zanzibar tutaendeleza ushirikiano huo katika masuala ya mafunzo kupeana fursa za mitaji na ajira kama jinsi ambavyo Wizara hizi zimekuwa zikishirikiana kwa karibu sana kwa kipindi chote.

Kwa hiyo, tutaendelea ushirikiano huo mzuri na tunashukuru kwa wazo hilo ambalo umelitoa na sisi tutalifanyia kazi tuone namna gani bora la kuweza kulirasimisha na pengine hata ikilazimisha kubadilisha sera au sheria tutalifanyia kazi. (Makofi)
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; je, Serikali imejipangaje kutokana na miradi mikubwa ambayo inaendelea hapa kama Bwawa la Mwalimu Nyerere lakini pia na Miradi ya SGR; ili kuhakikisha vijana wetu wa Tanzania wanaenda kusimamia hii miradi pindi itakapokamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Ili kuendana na Uchumi wa Bluu; je, Serikali imejipangaje kufundisha vijana wetu kwenye mambo ya uvuvi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bonnah Ladislaus Kamoli, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari Serikali ilimeshaliona hilo na kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais na maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ile miradi wakati inaanza tayari tulishatambua vijana ambao walipaswa kuchukuliwa na kwenda kupata mafunzo zaidi. Katika Mradi wa Reli ya Kisasa, vijana 3,526 tayari walishaajiriwa. Kati ya hao, tumewatambua vijana 1,916 ambao wataenda kwenye vyuo vyetu mbalimbali na ndio watakaofanya succession plan kwenye maeneo hayo kwa ajili ya masuala ya teknolojia na ufundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, likiwa sambamba na Bwawa la Mwalimu Nyerere ambapo ni zaidi ya vijana wa Kitanzania 10,228 ambao tumewaajiri, kati hao 146 tumeshawatambua na tutawasajili kuweza kuwajazia na kuwajengea ujuzi na skills za kuweza kuendelea hata baada ya watalamu wa kigeni wale kuondoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili katika succession plan; sheria yetu inaendelea kusimamia seccession plan ya local content ili ilete faida zaidi kwa Watanzania hasa katika kununua bidhaa za ndani na pia kupata wafanyakazi wa Kitanzania kwenye miradi hii ya maendeleo na kuweza kujeza kujenga uchumi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kuhusiana na Blue Economy, tayari kupitia Wizara yetu ya Uvuvi, wapo vijana ambao wanapata mafunzo na ufugaji wa samaki umeshaanza, ufugaji wa vizimba kule Mkoa wa Mwanza, pia tunafanya kwenye maeneo ya bahari ikiwa ni pamoja na Tanzania Zanzibar, tayari programu hii ipo, imeshaanza kufanya kazi na Mheshimiwa Rais ameendelea kutoa fedha kwa ajili ya kuwawezesha vijana hawa kwa kujiandaa na uchumi wa kisasa, ahsante. (Makofi)
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika,nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali; nina maswali mawili ya nyongeza.

i. Serikali inatumia mfumo gani kutathmini tija na matokeo ya programu hizo hasa ukizingatia kasi kubwa ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia iliyopo sasa?

ii. Serikali ina makakati gani wa kuhakikisha kwamba Vijana wengi wananufaika na programu hizo ukizingatia uhitaji ni mkubwa kuliko nafasi zinazopatikana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI, MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, ameuliza maswali mawili ya nyongeza; la kwanza ni kuhusu mfumo wa namna gani tunafanya tathmini kwa vijana hawa. Chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ipo Idara ya Maendeleo ya Vijana. Chini ya mkurugenzi huyo kuna timu maalum ambayo inafanya tathmini ikiwa ni pamoja na kuweka mifumo na utaratibu wa kuweka kanzidata katika vyuo husika ambavyo tunawapitisha vijana hao kupata mafunzo. Kwa hiyo tunabaki na takwimu kwa ajili ya kuwawezesha pia baada ya mafunzo waweze kupata fursa za ajira lakini zaidi tunawapa pia hadi vifaa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika,kuhusu swali la pili nalo ameuliza kuhusu vijana, sikuweza kulipata vizuri nikuombe kwa ridhaa yako, niweze kulisikia vizuri.
MHE.NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha vijana wengi zaidi wananufaika na programme hizo ukizingatia uhitaji ni mkubwa kuliko nafasi zinazopatikana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya mikakati ambayo Wizara imeweka ni pamoja na huo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya kuhakikisha vijana wengi wanaingia kwenye blue economy, kwa maana ya ufugaji wa samaki. Mkakati mwingine ni huu wa ukuzaji ujuzi ambapo tayari tumefundisha vijana zaidi ya 74,598, lakini pili upo mkakati mwingine huu ambao uko chini ya Wizara ya Kilimo unaoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu wa BBT ambapo tayari vijana 821, na Mheshimiwa Rais alizindua programme hiyo.

Meshimiwa Naibu Spika, tunao mkakati mwingine kupitia NACTVET pamoja na mafunzo ya TEHAMA ambayo tunaendelea nayo. Vilevile tuna Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa ambao unatutaka tuweze kuwafikia vijana zaidi ya 681,000 kwa kipindi hiki katika mpango huo wa miaka mitano. Tayari Serikali imeanza engagement na wadau wa maendeleo wakiwemo GIZ, International Labour Organisation pamoja na wadau wengine ni pamoja na Serikali yenyewe katika kuweka fedha kuhakikisha mafunzo haya tunayatoa kwa vijana walio wengi zaidi na kuwatafutia ajira ndani na nje ya nchi, ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hatua zote za uanzishwaji wa mfuko huu zilikwisha kamilika, ninaomba kufahamu tathmini iliyoelezwa kwenye jibu la msingi itakamilika lini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa mfuko huu kwa watu wenye ulemavu, Serikali inaonaje ikauacha mfuko huu ujitegemee kuliko kuuunganisha na mifuko mingine? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tathmini inayofanyika kwa sasa lilikuwa ni suala tu la kibajeti na kwa mwaka huu wa fedha tunakwenda kulikamilisha hilo kwa sababu tayari mipango yote imekwisha kukamilika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili la mfuko kutokuunganishwa na mifuko mingine. Ni kweli lakini pamoja na hilo tunatambua kundi hili ni muhimu sana na ni kundi ambalo ni maalum. Kwa umaalum wake tumekwisha kuona katika eneo la tathmini ni pamoja na kutambua kwanza vyanzo vya mapato na sera na sheria ambazo zitaongoza mfuko husika.

Mheshimiwa Spika, tatu, ni usimamizi wa fedha hizo, na nne, ni jinsi gani ambavyo fedha hizi zinazopatikana, zipo zitakazopatikana kutokana na ruzuku ya Serikali, lakini kwa sababu ya umaalum wake, zipo fedha ambazo zitatokana na wadau ndiko huko kunakopeleka umuhimu wa baadhi ya mifuko kusimama yenyewe kwa sababu msingi wa mfuko huu unaanzishwa na Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 ambayo inataka uwepo wa mfuko huu. Kwa hiyo, kuna mifuko ambayo baada ya tathmini haitakuwa imeungwanishwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya tathmini tutakuwa tumepata picha kamili ya namna ya kuongoza mfuko huu ili uweze kuleta tija na faida zaidi kwa ndugu zetu watu wenye ulemavu, ahsante.
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, kwa kuwa watu wenye ulemavu wameonekana mara nyingi wakiwa wanaombaomba na wakati mwingine kutumiwa kama chambo katika kuomba; je, ni mkakati upi wa Serikali katika kuwasaidia watu hawa kujikwamua kiuchumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu namna ya kuwasaidia watu wenye ulemavu kutokana na suala la kuwa ombaomba. Moja ya mikakati ya Serikali ni kutoa elimu; kumekuwa na changamoto sana ya kubadilisha mindsets za watu wetu. Na slogan ya Serikali ambayo inatumika hapa ni disability is not inability; kwa hiyo tumekuwa tukitoa elimu. Sambamba na hilo, Serikali imefungua vyuo vya watu wenye ulemavu ili kuwawezesha waweze kupata ujuzi wa ufundi stadi.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tumekwenda pia kwenye hatua nyingine ya kuweza kutoa mikopo kupitia halmashauri, asilimia mbili, kuwawezesha watu wenye ulemavu. Sambamba na hilo pia tumekwenda katika hatua nyingine ya kuhakikisha kwamba tunawasaidia watu wenye ulemavu katika kutengeneza miongozo mbalimbali ukiwemo huu wa kuweza kuwa na mfuko maalum pamoja na kuwawezesha na kuwaweka kwenye vyama ambavyo vitawasaidia kuweza ku-raise agenda zao na kuweza kusaidiwa na Serikali kwa ukaribu na kwa umoja zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hilo la kuendelea kuwa na suala la ombaomba, tayari tumeshaweka mikakati mbalimbali ikiwemo kuweza kuongeza fedha katika mifuko ya watu wenye ulemavu ili waweze kupata elimu ya ujasiriamali na kujikwamua zaidi.

Mheshimiwa Spika, upande wa elimu, tayari tuna inclusive education ambapo kwa wale wenye uwezo wa kwenda shule Serikali imekuwa ikiwachukua. Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wetu, amekwisha kutoa zaidi ya bilioni tatu kwa ajili ya kurekebisha vyuo vya watu wenye ulemavu na kutoa huduma za utengemavu, ahsante.
MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika nashukuru sana, ningeomba kujua kwenye hii Wizara ilitolewa milioni 60 kwa ajili mafuta ya watu wenye uarubino. Nataka nifahamu ni lini sasa yale mafuta yataanza kusambaa Tanzania nzima, kwa sababu nina amini kuna Wabunge hapa wananiuliza kila siku wanahitaji haya mafuta? (Makofi)
NAIBU WAZIRI OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE.PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa
Spika, hili ni la kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu aliona umuhimu huo. Tulikuwa tunapata mafuta kutoka nje ya nchi sasa yanatengenezwa pale KCMC, na gharama zinalipwa na Mheshimiwa Rais wa Serikali ya Awamu ya sita. Suala la usambazaji na ufikaji wa mafuta ni suala la uratibu tu ambalo nitaomba Mheshimiwa Mbunge niwasiliane naye kama kuna changamoto sehemu za wao kuweza kuyapata; lakini pia tutaweka utaratibu wazi wa kuweza kuona ni namna gani kila eneo wataweza kuyapata mafuta haya muhimu kwa ajili ya watu wetu wenye ulemavu, ahsante sana.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika ahsante sana, kwa kuwa matibabu ya watu wenye ulemavu ni ya ghali sana kwa namna ya kuwapeleka hospitali lakini na hata matibabu yenyewe.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka ruzuku ya bima ya afya kwa ajili ya watu wenye ulemavu ili kuwapunguzia adha wazazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa
Spika, ahsante, moja ya jitihada za Serikali ni pamoja na kuandaa mwongozo huo wa mwaka 2020 ambao umekamilika katika kuona na kuratibu masuala ya changamoto, kwanza kutambua changamoto za watu wenye ulemavu lakini pili kuona namna gani tunaweza kuwahudumia zaidi. Kwa hiyo kuwepo kwa mfuko wa watu wenye ulemavu utatatua changamoto nyingi sana ambazo zitasaidia sana kuona namna gani tunaenda kutatuta changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la bima, kwa kuwa tuko kwenye utaratibu sasa wa kupata universal health care, mfuko wa bima ya afya kwa wote tutaona pia umaalum wake kwa sababu kundi hili ni muhimu kuweza kuliangalia kwa umaalum wake na kulifanya hilo. Kwa hiyo niseme tu nimepokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na kwamba tutaufanyia kazi, ahsante sana.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza. Pamoja na majibu ya Serikali, tunatambua kwamba nchi hii hujengwa na wafanyakazi ambao wameajiriwa na wafanyakazi ambao hawajaajiriwa kwa mfano wakulima na wafugaji.

Je, sasa Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia hawa watu ambao wameijenga nchi yetu kwa muda mrefu wakiwa hawajaajiriwa kwa kazi za Serikali kwa maana ya wakulima na wafugaji ili kuwasaidia wanapofikia umri ambao hawawezi kufanya kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali inapaswa kuzingatia Watanzania wote wanaojenga nchi yao katika kufanya kazi mbalimbali. Moja ya mikakati ya Serikali ambayo iliona suala hilo ambalo Mheshimiwa Mbunge amelisema, ni pamoja na kubadilisha skimu za utoaji wa pensheni katika mifuko ya hifadhi ya jamii na kuzingatia kwamba yapo makundi ambayo siyo ya wafanyakazi, wanafanya kazi zisizo rasmi, lakini wanafanya kazi kwa mfano kwenye maeneo ya viwanda, kilimo, biashara na wajasiriamali wadogo wadogo. Tayari Mfuko wa NSSF ambao unashughulika na sekta isiyo rasmi umeanza kukusanya michango kwa kuwatambua hawa walio kwenye makundi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, bado Serikali pia kwa kutambua kwamba wapo ambao ni wajenzi wa Taifa na wakifikia katika hatua ya uzee wanahitaji msaada. Serikali imekwisha kuandaa vituo vya wazee ambao wanakuwa wanahitaji msaada wa Serikali kwa mfano wa matibabu na maisha, kuna mpango maalum wa TASAF ambapo zaidi ya wazee 647,512 ni wanufaika wa mfuko huo. Lakini zaidi ya hapo pia vipo vituo maalum zaidi ya 14 katika mikoa 26 nchini ambavyo Serikali imeviweka kwa ajili ya kuwasaidia wazee, ahsante sana.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa kumekuwa na malalamiko mengi yanayohusu huduma mbalimbali za wazee ikiwemo tiba na mengineyo. Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kuleta Sera ya Wazee Bungeni ili kwa ujumla wake tuangalie mapungufu na yale ambayo yanaweza kufanyika kuweza kujenga mazingira mazuri ya wazee wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze kwa swali zuri ambalo limeendana kabisa na mpango wa Serikali ambao tunaufanya hivi sasa. Katika vituo hivyo vya wazee, na katika utaratibu uleule wa kuangalia makundi ambayo yanahitaji msaada zaidi, hasa katika masuala ya chakula, malazi, mavazi, matibabu na welfare yao kwa ujumla, tayari Sera ya Wazee ipo na iko katika hatua za kwenda kufanyiwa marekebisho ili kuweza kuhakikisha tunawasaidia wazee hawa, ikiwa ni pamoja na kuunda mabaraza ya wazee katika ngazi za halmashauri huko mpaka ngazi ya vitongoji, mitaa na vijiji ambayo tayari imekwisha kuanza kufanya kazi na zinafadhiliwa na halmashauri zetu kote nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kikokotoo, issue siyo elimu, issue ni ile percent inayotolewa. Watu wanalalamikia percent inayotolewa kwamba hawajakubaliana nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; tuna malalamiko kutoka kwa kundi muhimu la wafanyakazi ambao wote tunajua historia ya wafanyakazi ndiyo hasa kundi kubwa lililokuwa likifanya mapinduzi mbalimbali, sehemu mbalimbali duniani. Sasa ni lini Serikali pamoja na majibu iliyoyatoa, itafanya ile ujumuishi? Kwa sababu wafanyakazi waliostaafu pia wanasumbuka sana. Wapo ambao walikuwa NSSF wakahamishiwa PSSSF, wanapokwenda kudai mafao yao wanalipwa kidogo na PSSSF na wanatakiwa tena kuanza kufuatilia NSSF; imeleta usumbufu mkubwa. Ninyi kama Serikali mmejipangaje kuwasaidia ili walipwe kwa pamoja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Askari wetu au Jeshi la Polisi, wao ni kama majeshi, lakini kikokotoo hiki kinaoneka kwamba hakiwahusu majeshi mengine, isipokuwa askari wameingizwa kwenye kikokotoo hiki, nao hawakubaliani na hiyo. Wanasema kwa nini wao wasiwe regarded kama majeshi mengine yalivyokuwa regarded? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Msambatavangu alivyoeleza, ni kwa sababu tu ya pengine taarifa kuwafikia watu vizuri na ndiyo maana wakati wote kumekuwa na mkakati wa kutoa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali watumishi waliokuwa wakichangia kwa asilimia 25, kama alikuwa anapata shilingi milioni 46, kwa sasa malipo ya mkupuo analipwa shilingi milioni…; wakati huo alikuwa analipwa shilingi milioni 44 na katika pensheni ya kila mwezi alikuwa analipwa shilingi 800,000. Kwa mabadiliko haya ya sasa ambayo yalikubaliwa na wadau wote pia wakiwemo vyama vya wafanyakazi, katika asilimia 33, ukiangalia mkupuo umeongezeka. Ukiangalia mchango wake ule wa milioni 46 sasa hivi analipwa milioni 58. Pia ongezeko lingine kwenye pensheni ya kila mwezi, analipwa zaidi ya shilingi 700,000. Kwa hiyo, unaweza ukaona utofauti ambao umekuwepo hapo katika hiyo. Umekuwa na faida. Zaidi ya asilimia 81 kwa sasa wananufaika na mpango huu. Lilifanywa hili baada ya kushirikisha wadau, kwa sababu asilimia 31 ndio wamekuwa wanufaika wa kikokotoo hiki kipya. Kumbuka tulikuwa asilimia 25, tumekuja asilimia 33.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna faida nyingine ya kutengeneza uendelevu wa mifuko. Hii mifuko utakumbuka, awali kulikuwa kuna mifuko mingi; LAPF, tulikuwa tuna PSSF, na mifuko mingine mingi. Wajibu wa Serikali na agizo lililotolewa ilikuwa ni kuangalia ile faida kwamba hii mifuko itakuwa inaendeshwa lakini mwisho wa siku wanachama wake wapya hawawezi kunufaika nayo kwa sababu ya kutokuwa na ustahimilivu au stability ya mifuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kilichofanyika ni kuunganisha mifuko ili kutengeneza utaratibu ambao utawasaidia zaidi wanachama kuweza kunufaika na ndiyo maana tukawa na skimu hizo mbili. Moja ya upande wa wafanyakazi wa Serikali ambapo ni PSSSF na pili NSSF inashughulika na wale ambao ni watumishi katika kada za kawaida. Kwa hiyo, faida ni nyingi kuliko hasara kwa kipindi hiki. Walioongezeka hapo ni asilimia 81 ambao wanapata faida zaidi hasa kwenye mkupuo ule wa mwisho, imekuwa fedha wanayolipwa kwenye mkupuo ni kubwa zaidi, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Waziri kuna viwanda katika Mkoa wa Pwani sehemu za Mbagala na sehemu za Mkuranga wanawapa wafanyakazi shilingi 4,000 kwa siku. Mfanyakazi anaingia saa mbili asubuhi anatoka saa 11 jioni anapata ujira wa shilingi 4,000; je, hii ni sawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali mnasimamia vipi matajiri na waajiri wakubwa ambao wanadaiwa madeni na wafanyakazi kwa muda mrefu. Makampuni ya Chai ya Rungwe, Kampuni ya Kiwira Coal Mine na Kampuni ya TANESCO waliokuwa vibarua takribani sasa ni miaka mitano hawajapata fedha zao.

Je, Serikali mnasimamiaje suala hilo kuhakikisha watu hawa wanapata haki ambayo wanastahili waliyoitendea kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la kwanza la Mheshimiwa Mbunge ni kweli tumeendelea kufanya kaguzi, kwa mujibu wa sheria ipo namna na mikataba ya kazi ambayo inatambua aina ya ajira mtu anayoifanya. Wapo wanaofanya kazi kwa maana ya permanent and pensionable kwa maana ya mkataba unavyoeleza lakini pia wapo wanaolipwa kwa mpango wa wiki moja, kila baada ya wiki, wapo wanaolipwa kila baada ya mwisho wa mwezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo hayo, imebainika ndiyo moja ya tatizo ambalo tumelibaini Mheshimiwa Mbunge ni kwamba, wapo waajiri ambao wamekuwa wakikwepa kuwapa mikataba ya kazi wafanyakazi hawa ili kuendelea kuwaita vibarua na wakafanya kazi kwa muda mrefu. Huo ni unyonyaji mkubwa na Ofisi ya Waziri Mkuu tayari tumekwishaanza kuchukua hatua na tunafanya kaguzi, tunaenda kuangalia historia wafanyakazi wamefanya kwa kipindi gani na ni aina gani ya kazi anayoifanya ili kuweza kuhakikisha tunawaingiza kwenye mfumo wa kuwa na mikataba ya kazi ili haki zao ziweze kulindwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni lile linalohusiana na udhulumaji ambao unafanyika au kutokulipa maslahi ya wafanyakazi. Vivyo hivyo katika Sheria ya Ajira na Mahusiano kazini inaeleza moja ya mambo ni kukubaliana katika mkataba, yaandikwe na yaainishwe wazi. Kitendo cha waajiri kutokuwalipa mishahara au maslahi yao ni kuvunja Sheria ya Ajira na Mahusiano kazini lakini sambamba na hilo, ndani ya mkataba kuna masuala ya Pay As You Earn kwa maana ya kodi ya Serikali. Maana yake asipolipwa maana yake anakwepa pia kodi ya Serikali, pia kuna kipengele ambacho ni cha lazima cha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, asipolipwa mshahara maana yake anakwepa pia kupeleka fedha kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu kipo kipengele cha WCF kwa maana ya workers compensation. Kama halipwi mshahara maana yake hiyo pia ni eneo ambalo anakosa haki hiyo ya kuweza kulipwa, sambamba na hilo sheria nyingine tumeendelea kuzichukua na tunawapeleka mahakamani kwa summary suits maana yake hana muda wa kujitetea na hatua tunazichukua na sasa yapo mashauri ambayo tunaendelea nayo, hivyo kwenye maeneo hayo mahsusi nitaomba pia aniambie ni wapi ili tuweze kushirikiana naye kuweza kuchukua hatua. Ahsante. (Makofi)
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mufindi Kampuni ya Ekaterra imeinunua Kampuni ya UNILEVER jambo ambalo limeacha malalamiko makubwa ya wananchi kukosa stahiki zao. Je, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu haioni umuhimu wa kuwasaidia wananchi hawa kumaliza malalamiko yao, ikiwa ni pamoja na kufika pale ili waendelee kunufaika na Taifa lao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kihenzile kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwamba suala hili Mheshimiwa Kihenzile amekuwa analifuatilia kwa muda mrefu la kampuni hiyo ya UNILEVER baada ya kuingia mkataba wa kwamba sasa kampuni inakuwa winded up na kuchukuliwa na kampuni nyingine. Utaratibu uliopo kampuni inaponunuliwa au inapoenda kufilisika wajibu wa kwanza ni kuhakikisha wametambua madeni lakini pia kwa maana ya liabilities pamoja na assets zilizopo. Kwa wafanyakazai hatua ya pili itakuwa sasa ni kulipa madeni ikiwemo madeni ya wafanyakazi kwenye kampuni husika, hata kama kuna transfer ya umiliki, jambo la kulipa madeni ambayo ni liabilities ni la msingi na ni la kuzingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo kwenye eneo hili la kesi ya UNILEVER Mheshimiwa Mbunge nimueleze tu kwamba kuna hatua mbili ambazo Ofisi ya Waziri Mkuu ilichukua. Hatua ya kwanza Kamishna wa Kazi alikutana na wafanyakazi hao na kuchukua malalamiko yao. Wapo ambao walifukuzwa kazi wakati huo bila kufuata utaratibu wa retrenchment tuliagiza warudishwe kazini. Pia lipo kundi la pili la wafanyakazi ambao walilipwa walikuwa zaidi ya 500 na hatua ya tatu kundi la tatu kwenye wafanyakazi hao ni wale ambao bado maslahi yao yalikuwa hayajaelezeka vizuri, wapo ambao walikuwa wana mikataba na wasiokuwa na mikataba.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ambayo tumeichukua tuliwaelekeza waende CMA ambapo shauri linaendelea mpaka sasa katika Mahakama ya Kazi na hatua ya tatu ambayo tunaenda kuichukua ni kuhakikisha baada ya maamuzi ya CMA na wale ambao walikuwa bado hawajaainishwa kwamba wako kwenye eneo gani la vipengele vya mikataba, wakutane na Kamishna wa Kazi ili haki zao ziweze kulindwa. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu lilikuwa linasema faida na hasara ya uwekezaji. Umeniambia kiasi cha uwekezaji kilichowekezwa lakini hujaniambia faida na hasara ya kifedha. Kwa sababu inasemekana kwamba uwekezaji unafanywa kwenye maeneo yasiyokuwa na tija. Kwa hiyo, naomba nijibiwe swali la faida na hasara ya kifedha. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, moja ya miradi mipya ni mradi wa Mkulazi kwa ajili ya uzalishaji wa Sukari. Pia, kwa mujibu wa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambae wewe umemrejea anasema, Mipango duni ya utekelezaji wa mradi huu mpya ambao fedha za mifuko zinatumika, umesababisha gharama ya uwekezaji kuongezeka kwa bilioni 79, moja, hasara ya miaka ya miwili mfululizo ya bilioni 20.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, unadhani mna matatizo gani linapokuja suala la uwekezaji kwa kutumia fedha za mifuko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kuhusu swali lake la kwanza kuhusiana na faida na hasara lilikuwa linauliza tangu kuanzishwa kwa mifuko ni kiasi gani cha fedha kimewekezwa na lakini eneo la pili, lilikuwa linauliza katika kila mfuko nini faida na hasara za uwekezaji? Kwa hiyo, ilikuwa ni faida na hasara sio fedha. Hata hivyo, tumeeleza kwenye eneo la fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la fedha miradi ambayo imewekezwa nimeeleza kwenye swali la msingi kwamba ni zaidi ya shilingi trilioni 14. 4 ambayo imewekezwa katika mifuko miwili kwa maana ya PSSSF zaidi ya shilingi trilioni 7.4 lakini pia kwenye NSSF ni trilioni 6.3. Sasa kwa fedha ambazo ni hasara haiwezi kuwa counted ni hasara kwa sababu uwekezaji ule ni endelevu na umeendelea kuwa wanaendelea kulipa kila wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika principle za uchumi ni sawa na kupwa na kujaa kwa bahari. Wakati wa uwekezaji tunaofuata ni mwongozo unaotolewa na Benki kuu ya Tanzania ambayo inaeleza maeneo ya uwekezaji. Pili, inaeleza namna gani ambayo watakwenda kuwekeza pamoja na ukomo wa kiwango cha kuwekeza fedha hizo. Kwa hiyo, hiyo unaweza ukaja ukaiona katika miradi na mingine imekuwa inawekezwa ikiwa ni inatoa huduma kwa wananchi. Kwa mfano; daraja la kigamboni na majengo mengine ambayo ni ya mifuko hii yameendelea kupata fedha kulingana na hali ilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye swali lake la pili ambalo ameuliza kuhusu uwekezaji kwenye mfuko wa Mkulazi na ameeleza kuhusiana na Taarifa za CAG. Msingi ni ule ule kwamba Mkulazi kwa sasa hatujaanza uzalishaji lakini katika maeneo yale yaliyoainishwa utakumbuka vizuri wakati wa Uwekezaji BOT inatoa kanuni na miongozo na inaeleza maeneo ya uwekezaji na tatu inaeleza hadi ukomo wa uwekezaji.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Serikali ina mpango gani wa kuwanyanyua vijana hawa wa skauti walioiva kimaadili na kizalendo, kuwatengea mgao maalum wa kupata ajira zinapotokea kama vile kwa Jeshi la Wananchi na taasisi nyingine?

Mheshimwia Mwenyekiti, swali la pili: Serikali ina mpango gani wa kutenga ruzuku malalum kwa ajili ya shughuli za Skauti Tanzania?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kwa vijana walioiva kiuzalendo ambao wanatoka skauti, na mara nyingi tumekuwa tukiwaangalia sana kwenye suala la ajira, na ajira hizi pindi zinapotokea ziwe za Serikali na pia kwenye taasisi na vyombo vyetu vya usalama, imekuwa ni moja ya sifa ama kigezo, kama wale walioenda Mgambo na JKT kuangaliwa kama sifa ya ziada. Kwa hiyo, tumekuwa tukiwaingiza kwenye vyombo vyetu vya ulinzi na usalama na pia katika majukumu mengine ambayo yanatokana, au ajira zinazotoka upande wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuhusu ruzuku; Skauti Tanzania imeanzishwa kwa mujibu wa sheria, na bahati nzuri kabisa, Skauti Mkuu Tanzania ni Amiri Jeshi Mkuu ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Kwa hiyo, katika utaratibu wa masuala ya kuwawezesha, kama jinsi sheria ya kuwaanzisha wao inavyoeleza, ndivyo hivyo hivyo wanaweza kupata pia fedha kupitia mifuko mbalimbali ambayo inasaidia kama sehemu ya chombo ambacho ni kama Jeshi, yaani inafanana na ile ambayo ipo katika Jeshi la Mgambo. Kwa hiyo, msaada, na pia iko fedha inayotoka Serikalini na kuna fedha ambazo ni kutoka kwa wadau mbalimbali huzitoa kupitia mifuko hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutazidi kuangalia kuweza kuboresha zaidi maslahi ya Skauti wetu kwa sababu wamekuwa wakifanya kazi kubwa na hasa kwenye masuala ya uokoaji pale yanapotokea majanga, sherehe za kitaifa na majukumu mengine, ahsante.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia fursa hii. Kwa kweli vijana wetu wa skauti wametapakaa takribani nchi nzima; Bara na Visiwani. Kama Mheshimiwa Waziri alivyokiri kwamba wanafanya kazi kwenye maeneo mbalimbali. Je, Serikali haioni haja sasa kutenga mfuko maalum wa kibajeti kupitia Wilaya, Mkoa na Kitaifa zaidi ili wawe na uhakika wa fedha zao kwa ajili ya kuendesha programu zao pamoja na kufanya kazi zao kiujumla? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Usonge ambalo limefanana pia na jibu langu la msingi, na hata swali alilouliza Mheshimiwa Asha kwenye suala la kibajeti, kwamba tayari wao wana sheria ambayo inaanzisha na inatoa taratibu ikiwa ni pamoja na masuala ya kifedha, lakini kwa sababu pia ni eneo ambao linaonekana pengine lina upungufu, tutauangalia na Serikali na kuweza kuona pale panapopelea tuweze kuwasaidia zaidi na kutengeneza mifumo ambayo itawasaidia kuweza kuratibu na kutekeleza majukumu yao kama ambavyo jinsi tunawatarajia, ahsante.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa mujibu wa sensa, wazee wako asilimia 5.7 tu, idadi hii ni ndogo sana ikilinganishwa na umuhimu na mchango mkubwa wa wazee hawa katika Taifa hili. Je, Serikali haioni haja na umuhimu wa kutenga chanzo kimoja mahususi kwa ajili ya pensheni ya wazee hawa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni pamoja na upande wa Zanzibar. Kwa kuwa wazee wa upande wa Zanzibar wanapatiwa pensheni kwa wazee wote, ni kwa nini Serikali inachukua muda mrefu wa kufanya utafiti tusijifunze kwa wenzetu wa Zanzibar, japo kuanza na wazee wa umri wa miaka 70 ambao kwa mujibu wa sensa wako asilimia 2.7 tu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wazee kwa mujibu wa sensa ni kweli ni asilimia 5.7, lakini katika kuangalia umuhimu huo wa wazee na ndiyo maana nikasema kwenye jibu la msingi kwamba Serikali itaendelea kufanya utafiti na kuangalia best practice ya uwezekano pia wa Serikali wenyewe kuangalia katika masuala ya kibajeti kama inaweza kuhudumia kundi hili.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tayari hata ukiangalia kwenye swali lake la pili ambalo linaelezea kufananisha ulinganifu wa upande wa Tanzania Zanzibar, kwamba wazee wamekwishaanza kulipwa, vivyo hivyo, ni mambo yote haya ya kifedha ambayo katika kuangalia lazima tuone namna ambayo tunaweza tukapata fedha za uhakika kuwalipa wazee hawa.

Mheshimiwa Spika, wazee waliokuwa wanafanya kazi wamejumuishwa kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na katika Mifuko hiyo kuna skimu maalum ambayo inaruhusu sasa mtu yeyote, hata akiwa hajaajiriwa, kutoa michango yake katika mifuko hiyo na baadaye kuja kupata pensheni yake.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, niseme tu kwamba katika utafiti ambao tunaufanya kwa kipindi hiki, haitachukua muda ili kuweza kuliangalia ikiwa ni zingatio, kama jinsi ambavyo Serikali inatambua mchango wa wazee hawa, umuhimu wao, lakini pia kama chemchemi ya busara na waliochangia kwa sehemu kubwa uchumi wa Taifa. Kwa hiyo tumewaangalia pia na tumeendelea kuweka utaratibu kama huu wa TASAF wa kuwapa fedha ambapo kaya maskini wanasaidiwa wazee hawa, lakini pia kuna taratibu za utoaji wa mikopo ambazo nazo pia zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo wakati haya mambo yanaendelea sambamba na hilo, ni pamoja pia na kujiridhisha sasa kwenye masuala ya kibajeti kama tutaona umuhimu. Tutalileta kwenye Bunge lako Tukufu kwa ajili ya kupata ushauri, maoni na mapendekezo ya wadau, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri, kumekuwa na malalamiko kwa baadhi ya wazee katika maeneo mbalimbali wakiwemo wa Mkoa wa Mara, kwamba hawapati ile pensheni yao kwa wakati. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha wazee hawa ambao wamelitumikia Taifa wanapata pesa yao kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Amos Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niombe tu kwa sababu hilo ni suala mahususi kabisa la Mkoa wa Mara, niwasiliane na Mheshimiwa Mbunge niweze kupata taarifa za kwa nini ucheleweshwaji unafanyika kwa sababu ni jambo ambalo kwa sasa tunalipa kimtandao na taarifa zinapatikana kwa wakati na tumekuwa tukilipa kwa wakati kabisa katika kipindi hicho. Kwa hiyo jambo hili litakuwa mahususi, nimwombe Mheshimiwa Ester Bulaya anipatie taarifa hizo niweze kufanya ufuatiliaji mara tu baada ya Bunge hili, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Hili suala la upande wa Zanzibar kupata pensheni ya wazee wote na Tanzania Bara kukosa wakati ni nchi moja, naomba kujua, nini tamko la Serikali kuhusu wazee wa Bara ambao wanatakiwa kupata pensheni sawa na wazee wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kama nilivyojibu kwenye swali la msingi kwamba kwenye masuala ya kipensheni tayari tunayo Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, kwa hiyo mtu yeyote kwa sasa, hata kabla ya uzee, unaweza ukaanza kupeleka fedha.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa pili, kuhusiana na kwamba tutoe tamko; ni hilo la kufanya utafiti ili kuweza kujiridhisha uwezo wa Serikali katika kuhudumia wazee hawa.

Mheshimiwa Spika, tatu, suala hili tayari wazee wanahudumiwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa sasa tunavyo vituo 14 vya wazee wasiojiweza ambavyo ni vya Serikali, vinahudumia hawa wazee na vituo 15 vya watu binafsi na jumla ya wazee 496 wanapata huduma kwenye hayo maeneo.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, iliweka mpango wa TASAF ambao unanufaisha wazee. Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imeona bado pia kuna umuhimu wa kuwahudumia wazee, imeweka utaratibu wa mikopo, utoaji wa fursa na mitaji; Serikali hii hii imeweza kuendelea kuwaangalia wazee kwa kuwatolea huduma ya matibabu bure na kuna desks zaidi ya 588 kwenye hospitali zetu kwa ajili ya kuwahudumia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili suala Serikali inaliangalia kwa kina sana kuona namna gani wazee wetu tunawaenzi na kuwaheshimu katika mchango mkubwa walioutoa wakati wa ujana wao kuchangia uchumi wa Taifa. Ahsante.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wazee wengi ambao walikuwa wafanyakazi wa Shirika la Posta na Simu na ATCL na Mashirika mengine kama Reli, mpaka sasa hivi wanahangaika kupata vipensheni vyao. Je, ni lini Serikali itamalizana na wazee hawa ili wakifa wakapumzike kwa amani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kifo ni mpango wa Mungu lakini hatuombei itokee hivyo kwa wazee wetu, waishi na waendelee kudumu.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali hilo la Mheshimiwa Asha kuhusiana na wazee hawa waliokuwa watumishi wa Shirika la Posta pamoja na Reli kupata pensheni zao; itakumbukwa vizuri kwamba tayari kulikuwa na mashauri mbalimbali ya wazee ambao walikuwa wanafanya kazi kwenye mashirika hayo. Wapo tayari ambao wamekwishalipwa pensheni zao lakini pia wapo ambao wameendelea kuwa na madai. Hii imetokana zaidi na kutokuwepo kwa taarifa sahihi za madai yale lakini Serikali imeendelea kufanya ufuatiliaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe pia Mheshimiwa Mbunge, mama yangu Asha, baada ya hapa pia nipate taarifa ya madai hayo, kama kuna watu specific au mahususi tuweze kwenda kufanya ufuatiliaji kwamba wamekwama wapi katika kulipwa kama walikuwa kweli wafanyakazi halali, ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naishukuru Serikli kwa kuanza mchakato huu muhimu kwa nchi yetu, hata hivyo nina maswali mawili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mchakato huu wa kusajili Shirikisho la Kimataifa la Msalaba Mwekundu (IFRC)tumeambiwa uko kwenye mchakato kwa kipindi kirefu sana, takribani miaka thelathini sasa. Serikali sasa inatuambia mchakato utakamilika lini na mkataba kusainiwa ili shirika hili lianze kufanya kazi hapa nchini kwetu?

Swali la pili Serikali imejipanga vipi kulinda maslahi ya Watanzania katika mikataba itakayosainiwa ili kuhakikisha shirika hili la Kimataifa litakapoanzishwa ajira kwa Watanzania zitakuwepo kuliko kuajiri watu wa nje zaidi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI) K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Judith Kapinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze sana Red Cross Tanzania wamekuwa wakisimamia mchakato huu kwa muda mrefu sana kuweza kuhakikisha hata hatua hii inaweza kufikiwa na wamekuwa wakifanya kazi kubwa, kazi mbalimbali za Kitaifa, sherehe za Kimataifa, wakati wa maafa, pia wamekuwa wadau muhimu sana wa Serikali katika masuala ya maafa kwa hiyo ninawapongeza sana, pili ninawapongeza uongozi ambao umefanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ambalo ameeleza kuhusiana na kuchukua muda mrefu, kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi, tayari itifaki zote zimeshafanyika. Kwanza kuwasiliana na Shirikisho lenyewe; pili, kukutana na wadau na tatu, sasa iko kwenye hatua ya Wizara ya Mambo ya Nje katika kukamilisha tu itifaki za Serikali na taratibu za ndani ili kuweza kufanikisha jambo hili. Ndiyo maana tukasema kama Serikali kwamba sasa limefikia mwisho. Kwa hiyo, nawapongeza sana kwa hatua za ufuatiliaji.

Mheshimiwa Spika, pili, swali lake la kuhusiana na masilahi, ni kweli kwamba mashirika haya kimataifa yamekuwa yakija kufanya kazi nchini lakini tunaangaliaje ajira za wazawa?

Mheshimiwa Spika, Bunge lako Tukufu lilipitisha Sheria hapa ya Mwaka 2005 inayoruhusu uratibu wa ajira za wageni. Imekuwa ni wakati wote, hata kwenye Sheria ya Usajili wa Makampuni Sura Na. 212 inaelekeza namna unaposajiliwa kama kampuni, taasisi au asasi za kiraia, sharti ni kwamba waajiriwe Watanzania. Inapotokea ameajiriwa mgeni ni pale tu ambapo aidha taaluma yake ni maalum sana, au ufahamu au knowledge aliyonayo ni adimu hapa nchini kwamba hatuwezi kumpata Mtanzania mwenye sifa hiyo. Kwa hiyo, nitoe agizo hapa kwa taasisi zote, mashirika ya Kimataifa pamoja na Makampuni ya kiuwekezaji ya nje yaendelee kuzingatia utekelezaji wa Sheria ya Mwaka 2005 ya Kuratibu Ajira za Wageni inayowataka waangalie matakwa ya ajira za Watanzania.

Mheshimiwa Spika, pia usajili wa IFRC utakuwa chini ya msukumo wa Red Cross Tanzania. Tutawaomba Red Cross nao waendelee kutusaidia kupata taarifa na kuratibu ili ajira za Watanzania zisipotee, ahsante sana.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Kwa kuwa kumekuwa na malalamiko mengi sana kuhusiana na kikokotoo hicho na inaelekea hakuna mpango wa kukirekebisha.

Je, Serikali imejipangaje hata hicho kiasi ambacho kinatolewa, kitolewe kwa wakati?

Swali la pili, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba wastaafu sasa hasa wale wanaopata kiasi cha chini, mathalani shilingi 100,000 kwa mwezi, wanaongezewa kiwango hicho cha chini cha pensheni kwa kadri ambavyo mishahara inavyoongezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Priscus Tarimo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosisitiza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba, ndiyo maana tunaendelea kutoa elimu. Suala la kwamba kuna malalamiko, wanufaika wa mifuko hii ya pensheni, katika utoaji wa fedha kulikuwa kuna changamoto ya uwiano wa utoaji wa mafao, pia kulikuwa na changamoto ya uendelevu wa mifuko, tulikuwa na changamoto pia ya mkupuo wa malipo, kwa sasa katika mkupuo wa malipo wanufaika ni asilimia 81 ya wanachama wote, asilimia 19 mafao yao ya kila mwezi yameongezeka.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa katika mkupuo wa malipo, wanufaika ni asilimia 81 ya wanachama wote, na asilimia 19% mafao yao ya kila mwezi yameongezeka. Pia katika kipindi hicho utaweza kuona kwamba katika malipo yale ya kila mwezi, ilikuwa wanaweza kulipwa kwa asilimia 50, lakini sasa yamefikia asilimia 67 ya malipo. Hayo ni maboresho ambayo yametokana na utafiti uliofanyika. Tulifanya actuarial valuation, kwa kuwa mifuko hii ilikuwa na hali mbaya.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka tulikuwa tuna mifuko mingi ya GPF, PSPF, LAPF na NSSF. Mifuko hii kwa ujumla ilikuwa inashindana kwa wanachama wale wale. Utaratibu na maamuzi ya kuiweka pamoja mifuko hii imeleta tija kubwa na sasa mifuko imetoka from loss making trend to profit making venture. Kwa sehemu kubwa utaweza kuona, katika utaratibu huu, ndiyo maana tunaendelea kutoa elimu kwa sababu faida ni nyingi kuliko hasara ambazo zilikuwepo hapo awali.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tutaendelea kutoa elimu. Mheshimiwa Mbunge kama anadhani kuna watu wanalalamika, wote ambao wamekuwa wakifika kwa kutokuelewa utaratibu huu ofisini, wamekuwa wakipewa elimu na wameona faida hii. Namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama anao watu hao, nitashirikiana naye katika kutoa elimu kama jinsi ambavyo mifuko imeendelea kutoa, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa wako watumishi wa Serikali wakiwemo walimu ambao walikumbwa na mfumo huo wa kikokotoo wa muda katika kile kipindi ambacho kilianza kutumika, lakini mpaka sasa walimu hao mfumo wao wa pensheni haueleweki na hauko sawa: Nini kauli ya Serikali kuhusiana na walimu hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama alivyouliza kwamba mifumo ya ulipaji wa mafao ya walimu haueleweki.

Mheshimiwa Spika, huu utaratibu uliofanyika wa kuunganisha mifuko na kutengeneza uwiano sawa wa malipo haukuacha kundi lolote nje likiwemo kundi la walimu. Kwa hiyo, kama kuna sehemu ambayo anadhani kwamba kuna walimu wana changamoto hiyo, mimi nilipokee tu jambo hili kutoka kwake na nikalifanyie kazi, kwa sababu mfuko huu haujabagua kundi lolote katika kutengeneza maslahi ya wafanyakazi wetu, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika jibu ambalo Mheshimiwa Waziri ametoa, amesema wanufaika kwa sasa hivi wameongezewa pesa kwenye yale mafao ya kila mwezi, lakini lalamiko lao kubwa ni mafao ya mkupuo ambayo mmetoa asilimia 50 mpaka 30. Leo mtu anayestaafu ambaye angepaswa kulipwa shilingi milioni 100, anapata milioni 50. Huo ndiyo msingi wa swali: Ni lini mtaleta sheria mbadilishe ili wastaafu wapate asilimia 50 waweze kujikimu ili sasa wakipata hicho cha mwezi, tayari msingi utakuwa una maana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Nazidi kusisitiza kwamba suala hili ni la uelewa tu na elimu ambayo tutaendelea kuitoa. Mafao katika hatua ya awali katika Mifuko hii ya GEPF, PSPF, LAPF pamoja na PPF na NSSF, kila mfuko ulikuwa na aina yake ya utoaji wa mafao kulingana mfuko. Pia kwa hatua ya sasa, ukiangalia kwenye hili suala analosema la malipo ya Mkupuo, yalikuwa asilimia 25 na kwa mapenzi ya dhati Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kupitia vikao, mashirikisho ya vyama vya wafanyakazi sasa

hivi imefikia asilimia 33 ya ulipaji wa mafao hayo, hayakufika kwenye hiyo asilimia 50 ambayo anaisema kwenye hatua ya awali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jambo hili tutaendelea kutoa elimu bila kuchoka, na wanufaika ambao ni wanachama wenyewe hawajawa na tatizo kubwa hili. Kama wapo, nazidi kusisitiza kwamba Serikali tuko tayari kuwasikiliza na kuwahudumia ili kuweza kuhakikisha manufaa hayo wanayapata. Serikali hii inawapenda sana wastaafu na ndiyo maana maboresho yamefanyika kila wakati; kisera, kisheria, kimiundo, kimfumo na utoaji. Hata kwenye utoaji sasa tumeenda katika teknolojia ya tehama, ahsante. (Makofi)

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa kikokotoo ni kwa ajili ya watumishi na wastaafu; na uhalisia ni kwamba watumishi na wastaafu hawakitaki kikokotoo hiki: Ni lini Serikali italeta Muswada hapa wa kufuta kikokotoo hiki ili kuondoa kero kwa watumishi na wastaafu ambao hawakitaki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, no research no right to speak. Katika uhalisia wa actuarial report na utafiti uliofanyika, unufaikaji wa wanachama ni asilimia 81 ya wanachama wote, na asilimia 19, nadhani kama mtu atakuwa na hoja na hakubaliani, naye afanye utafiti na atuambie. Sisi tutaendelea kutoa elimu. Kwa kufanya hivyo, kwa sababu inaonekana suala linaanzia pengine kutokuwa na picha ya pamoja, tutaona umuhimu wa kuweka semina kwa ajili ya Wabunge ili kuweza kupata uelewa wa pamoja na kuwasaidia vizuri wanachama wetu kuliko kuwapotosha, ahsante.
MHE. MARIAM M. NYOKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, Serikali inatoa kauli gani kwa watumishi waliolipwa mafao pungufu hasa walimu; na wanapofuatilia wanaambiwa walipe gharama kwa ajili ya ufuatiliaji Dodoma? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam Nyoka, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa wastaafu ambao michango yao haikupelekwa, kwanza ni kosa kisheria, kwa sababu sheria zetu zinamtaka mwajiri kuwasilisha michango ya mwanachama kila mwezi, lakini pia kama kuna changamoto za hao wastaafu ambao wanaambiwa tena pia waanze kupeleka michango yao wenyewe, hilo naomba nilichukue na ni jambo serious nahitaji nilifanyie kazi siku ya leo, nikitoka hapa niongee na Mheshimiwa Mbunge kwa ajili ya hatua zaidi.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, napenda kuuliza: Ni lini Serikali itamaliza kabisa malalamiko ya wastaafu wa zamani wakiwemo wale wa Jumuiya ya Afrika Mashariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Masuala yote ya wastaafu tumeendelea sana kuboresha katika kuwasikiliza na pia kutatua changamoto zao. Hili suala la wastaafu wa Afrika Mashariki lilikuwa ni suala la kimahakama na Mheshimiwa kama unavyofahamu maamuzi ya Mahakama ndiyo huzingatiwa. Kwa hiyo, tutaangalia, wapo wengine ambao walikuwa kwenye hatua ya kufanya execution of decree ambayo ilitolewa na Mahakama na kulikuwa kuna hatua mbalimbali za kwenda kudai mafao hayo kwa waajiri. Kwa hiyo, liko katika utaratibu wa usukumwaji na ufuatiliaji kwa mfumo wa kimahakama, lakini kwa yale ambayo yamekuja upande wetu, tutaendelea kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, kama kuna issue substantial na specific kwa wastaafu kwenye eneo na jimbo lako, nitapenda nizipate ili tuzifanyie kazi. Kwa wote waliowahi kuleta, tumezifanyia kazi. Kwa hiyo, nawaomba sana, badala ya kusubiri, basi tutumie fursa hii kuweza kufanya hiyo kazi na kwenye semina ambayo tutaitoa tena kwa mara ya pili, itatusaidia sana kuweza kupata picha ya pamoja na kutatua changamoto hizi, ahsante.
MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza niseme kabisa Mheshimiwa Waziri sijaridhishwa na majibu haya, hii takwimu uliyoionesha hapa kwamba bado wastaafu 1,780 hawajalipwa lakini niende kwenye maswali mawili labda nitaridhika.

Sasa Mheshimiwa Waziri mnawatambuaje wastaafu ambao walistaafu miaka mingi wakahamia wengine vijijini, hawako kwenye mifumo hii ya kieletroniki na umesema wanafanyiwa uhakiki kuwatambua kupitia akaunti zao tayari wengine walishafungiwa na akaunti?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; hauoni ni kumweka mtu kwenye mazingira magumu sana ambaye anaitumikia Serikali wakati wake unapofika wa kustaafu halafu zinaanza chenga za kumlipa mafao yake.

Je, ungekuwa ni wewe ukamaliza Ubunge wako halafu mafao yasipatikane ungefikiriaje Mheshimiwa Waziri? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nicodemus Henry Maganga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza awali na anasema hajaridhika na majibu, lakini takwimu sahihi za Serikali chini ya mifuko na hizo kwamba wastaafu ambao wanalipwa ni hao 186,605 na kama ana takwimu tofauti basi tunamkaribisha ili tuweze kuangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili kuhusiana na suala la wastaafu ambao wako vijijini anasema masuala ya mtandao na kadhalika. Hao wanaendelea kuhudumiwa, katika ofisi zetu zote za mifuko na wanachama wale wamefunguliwa na hawa niliowataja wote wana akaunti hizo za benki na bado kuna desk ambalo linawahudumia wastaafu wetu na tumeajiri watu maalum kabisa wa kutoa huduma hiyo kwa wateja wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama ana jambo mahususi haliwezi kuwa la watu wote ni la hao watu wachache ambao anawasema na kama wapo anifikishie ili niweze kuchukua hatua zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni kuhusiana na kwamba ucheleweshaji wa ulipaji wa mafao, imebaki kuwa historia, tumeshafanya mabadiliko sasa hivi tunalipa kieletroniki na kuhusiana na mafao kama ni ulipaji kila mwezi kabla ya tarehe 25 tunalipa fedha hizo. Kwa hiyo, hilo ni suala la kihisroria analolielezea sasa hivi tumefanya mabadiliko makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii pia kuwaagiza Wakurugenzi na Mameneja wote wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii katika Mikoa waendelee kusimamia na kufanya lile suala la compliance kufatilia michango ya wanachama, lakini pili kuendelea kuhakikisha kwamba hakuna mstaafu yoyote ambaye anapata shida katika kipindi hiki, ahsante. (Makofi)
MHE. NANCY H. NYALUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, ni hatua gani Serikali imechukua kuhakikisha kwamba, inaondoa usumbufu kwa wanachama kupata mafao yao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, kwa nini Serikali imeamua kuunganisha Mifuko ya Pensheni, haioni kwamba, imechangia kuzaa changamoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA. VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Nancy, kama alivyouliza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wetu wa Hifadhi ya Jamii au Mifuko yote kwa pamoja PSSF na NSSF imeweza kwa sehemu kubwa sana kuondoa changamoto za ulipaji wa mafao kwa wakati. Kwa kufikia sasa tunalipa ndani ya siku 60 kama mfanyakazi atakuwa hana changamoto zozote za kitaarifa au kumbukumbu na hata wakati mwingine tunalipa hata chini ya siku saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine ambazo Serikali imechukua kupunguza usumbufu ni pamoja na kuweka Mfumo wa TEHAMA ambapo mwanachama anapata taarifa zake kupitia simu yake ya kiganjani na hatua nyingine mojawapo, pia ilikuwa ni hii ya kuunganisha Mifuko ili kuweza kutengeneza utaratibu wa uwiano katika malipo, lakini pia ulinganifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, lilikuwa ni katika kutoa usumbufu, kwa nini Mifuko iliunganishwa. Mifuko hii iliunganishwa, la kwanza kulikuwa kuna changamoto kubwa sana ya uwiano wa mafao. Mtu alikuwa PPF na aliyekuwa LAPF unakuta wote wamefanya kazi sawa na wamestaafu sawa na wametumikia Taifa sawa, lakini mmoja unaweza ukakuta katika pensheni yake mwishoni akalipwa milioni 40 na mwingine milioni 75 kwa sababu ya utofauti wa Mifuko, lakini kwa hiyo, kutengeneza ulinganifu wa mafao tukaona ni bora kuweza kuunganisha Mifuko hii baada ya kupata utafiti uliofanywa kama actuarial evaluation.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya pili, ilikuwa ni uendelevu wa Mifuko. Uendelevu wa Mifuko hii kwa sababu ya kuwa mingi ilikuwa inasuasua sana katika kujisimamia na kuwa na uendelevu wake. Mpaka sasa baada ya kuchukua hatua ya kuiunganisha thamani iliyokuwepo kwa PSSF ilikuwa ni trilioni tano, lakini sasa Mfuko umeweza kufika zaidi ya trilioni 8.1. Kwa hiyo, unaweza ukaona tofauti hiyo kubwa kama faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine ilikuwa ni kupunguza gharama za uendeshaji. Hii Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ilikuwa zaidi ya mitano, sasa unakuta yote ina Menejimenti, Bodi na huku kuna Menejimenti, lakini pia kuna Bodi, kuziendesha na kulipa mishahara, gharama za operational cost na kadhalika zote zilikuwa kubwa sana. Tumeweza kufanikiwa kwa Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kupunguza hasara hiyo ya gharama ya uendeshaji kutoka asilimia 12 mpaka asilimia tano.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Imekuwa vyema ambavyo mifuko hii inawekeza na kuwa na majengo ya kibiashara, lakini mfanyakazi ananufaikaje na biashara hizo? Pia tunajuaje wamepata kiasi gani na mwananchi wa kawaida anapokwenda kustaafu anapataje gawio sahihi katika Mifuko hiyo ambayo wamewekeza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA. VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni swali zuri la Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Sophia Mwakagenda. Ni kweli kwa kuangalia tija ya wanufaika wa Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii. Kile kinachochangiwa na mwanachama ukikipigia hesabu hata mwanachama yeyote kokote aliko akipiga hesabu ya fedha ambayo ameichangia mpaka kustaafu kwake na kile ambacho anaenda kukipata kama malipo ya mkupuo na kile anacholipwa mwisho wa mwezi ni kikubwa kuliko kile ambacho alichangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale waliokuwa katika Mifuko mingine unakumbuka PSPF wakati huo, lakini pia LAPF na NSSF fedha yake thamani imeongezeka ambayo ni ongezo kama faida ya uwekezaji na ulindaji wa thamani ya fedha kutoka asilimia 50 mpaka asilimia 67. Hii ni hatua kubwa sana ambayo Serikali imefanya na hata wenzetu nchi jirani, sitaitaja lakini, wamekuja kuiga mfano wa namna gani ambavyo tumekuwa tukiongeza maslahi ya wastaafu kutokana na uwekezaji unaofanyika katika mifuko, ahsante.
MHE. AMOUR KHAMIS MBAROUK: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nampongeza sana Waziri kwa majibu yake mazuri sana, Mwenyezi Mungu awawezeshe ila nina maswali mawili ya nyongeza.

Moja, hiyo mobile app ambayo iko asilimia 90 itakamilika lini ili kupunguza vifo vya wavuvi ambao wanakwenda kutafuta bila kujua wanatafuta nini na wapi? (Makofi)

Swali la Pili; hivi Serikali ilishawaeleza wavuvi wajibu wao kuhusiana na mobile app ambayo wanaingeneza? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y. WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Amour Khamis Mbarouk, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba, hii application tayari imekwishakamilika, iko katika asilimia 90. Asilimia 10 hiyo ni ile ya kuangalia ule mfumo unaweza kufanya kazi kwa usahihi kiasi gani. Halafu, hatua ya pili itakuwa inajibu swali lake la pili kwamba, wavuvi kama wamekwishakujulishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mfumo huu kuwa umekamilika, tutaanza hatua ya kuwajulisha wavuvi wote ili kuweza kunufaika na utaratibu huo, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wavuvi katika makundi mbalimbali. Ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, wakati wa hotuba ya Bajeti Kuu mwaka 2023/2024, Bunge hili lilipitisha Tozo ya shilingi 100 kwa kila kilo moja ya samaki wakavu aina ya dagaa wanaosafirishwa kuingia nchini au Kwenda nje ya nchi. Jambo hili limetafsiriwa vibaya Jimboni Ukerewe, jambo ambalo limefanya watumishi wanatoza wananchi shilingi 100 kwa samaki wanaosafirishwa ndani ya Wilaya jambo ambalo limeleta taharuki kubwa Jimboni Ukerewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka kupata kauli ya Serikali juu ya jambo hili ili kujenga amani kwa wananchi wa Jimbo la Ukerewe. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze, jambo hili amekuwa akilifuatilia sana kwenye Wizara ili kuhakikisha wavuvi waliopo katika ukanda huo wa Ziwa Victoria na pale Ukerewe wananufaika zaidi na biashara wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha marekebisha ya tozo, awali tozo ilikuwa kuanzia kilo 0 - 500 ilikuwa haitozwi chochote, lakini kilogramu kuanzia 501 na kuendelea ilikuwa inatozwa shilingi 100. Kwa kuzingatia kwamba ile ni biashara ya ndani na nje (import and export business) haiwezi kuwa na masharti sawa na ufanyaji wa biashara ndani ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ni kosa la kitafsiri la kanuni na sheria, hivyo natumia fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi kumwagiza Katibu Mkuu awasiliane na Mheshimiwa Mbunge ili kwenda kurekebisha changamoto hiyo inayowapata wavuvi wa hapo Ukerewe, ahsante. (Makofi)
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza; je, Serikali ipo tayari kugawa vifaa kwa wavuvi ili waweze kutumia hiyo mobile app? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Mwinyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza tangu awali kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali tupo tayari, ilikuwa kwanza ni kuangalia namna gani tunaweza tukawafanya wavuvi wetu waweze kunufaika na mazao ya bahari au mito na maziwa kwa kufanya huo utafiti na kupata hiyo application ambayo ni maalum inayosaidia wao kuweza kujua mazalia ya samaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, huu mpango ni pamoja na utaratibu wa kuweza kuwafundisha, kuwapa elimu, na pia utaenda sambamba na kuwapa vifaa. Zaidi hapa watatumia simu zao za mkononi tu kuweza kujua mazalia ya samaki na kupata taarifa zaidi. Kwa hiyo, tutaendelea kushirikiana nao na kuwawezesha kiutaalamu, kielimu, na kiujuzi katika kuhakikisha kwamba tunapata tija iliyokusudiwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kukuza sekta ya uvuvi. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tatizo linalowakumba wavuvi wetu nchini ni kukosa zana bora za uvuvi. Serikali katika bajeti yake ilisema itanunua meli za uvuvi ili igawe, ipeleke katika sehemu mbalimbali. Nataka kujua, mkakati huo umefikia hatua gani? Kwa sababu Mtwara kule sisi hatujapata hiyo meli. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika bajeti ilielezwa, lakini pia tumeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuwasiliana kwanza kwenye masuala ya fedha, kuhakikisha tunapata fedha na kutekeleza bajeti kwa kadri ilivyokuwa imepangwa kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, yale yote ambayo tuliyapitisha katika bajeti, tupo kwenye hatua za utekelezaji na tutahakikisha kwamba tunayatekeleza kama ambavyo tumekuwa na matamanio, likiwemo hilo la kuweza kununua meli na kuboresha katika sekta hiyo ya uvuvi kwa kuleta mitambo ya kisasa na pia kutumia teknolojia ya kisasa, ahsante. (Makofi)
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Ni lini Serikali itapunguza tozo ya shilingi 7,000 ambayo wavuvi wanatozwa wanapoingia kuvua samaki mle ndani ya Ziwa Rukwa? Ni lini sasa Serikali itakuja kupunguza tozo hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la lini Serikali itapunguza tozo, kwanza ni kupata uhakika wa aina ya tozo na kiwango kinachotozwa kwenye maeneo hayo. Kwa hiyo, naomba suala hili nilichukue kwa sababu linahusiana zaidi na takwimu ili kuweza kupata uhakika kwanza wa tozo zinazotozwa, na pili, kuweza kuona utaratibu wa kisera pamoja na kanuni na sheria zinasemaje katika eneo hilo na hatua ya tatu itakuwa ni kuleta mapendekezo ya kuona unafuu utapatikanaje kwa wavuvi wetu ili waweze kupata faida zaidi, ahsante. (Makofi)
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu ya mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza, kwa kuwa lengo kuu la hizi programu ni kutatua changamoto kubwa za vijana ikiwemo kukuza elimu ya ujuzi na kutatua changamoto ya ajira, kumekuwa na changamoto ya vijana wengi ambao wananufaika na hizi programu kushindwa kuunganishwa moja kwa moja na masoko ya ajira na mitaji pale wanapohitimu. Sasa, ni upi utaratibu au mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kuwa vijana hawa wanapohitimu programu hizi wanaunganishwa moja kwa moja na masoko ya ajira au mitaji ili wasirudi mitaani na kuondoa tija ya hizi programu wanazopata?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, bado kuna changamoto ya taarifa hasa kwa vijana wengi waliopo vijijini ya namna gani programu hizi zinapatikana, vigezo na utaratibu wa kuweza kupata programu hizi. Sasa ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha inaboresha mifumo ya taarifa ili vijana wengi wa Tanzania waweze kufahamu fursa hizi na kunufaika nazo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ng’wasi Damas Kamani kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upo utaratibu ambao Serikali inaendelea nao na tumekuwa tukiendelea kuufuatilia na kufanyia tathimini kuhusu namna ya kuunganishwa na ajira lakini pia kupata fursa za mitaji. Wote tutakuwa mashahidi kuwa kupitia Halmashauri zetu wapo Maafisa Maendeleo ya Vijana lakini pia Maafisa Maendeleo ya jamii. Wote hawa wanaendelea kutoa mafunzo kwa utaratibu wa mwongozo. Mikopo ya asilimia kumi kwanza inatangazwa lakini pili ni takwa la Ilani ya Chama cha Mapinduzi na tatu inaendelea kutangazwa katika Halmashauri zetu zote. Viongozi wengi sana na hata Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakihamasisha uwepo wa ile mikopo ya asilimia kumi. Pia ipo mifuko mingine ya uwezeshaji vijana ukiwemo Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambao upo Ofisi ya Waziri Mkuu na tumekuwa tunautangaza kupitia Mwenge wa Uhuru.

Mheshimiwa Spika, pia zipo programu nyingine katika wizara za kisekta. Ipo mipango ya kisekta ya kuwasaidia vijana kwa mfano kwenye masuala ya fursa za ajira, kuwaandaa kwenye ajira na mitaji. Pia tuna Wakala wa Ajira (TaESA) ambaye ana jukumu kubwa; kwanza la kuwatambua vijana wote wahitimu, pili kuwapeleka kwenye programu mbalimbali ikiwepo utarajali na kuwapeleka kwenye mafunzo mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Wizara zote za Kisekta zimekuwa na programu za vijana zinazohusiana na uandaaji wao wa kupata ajira hata ukiangalia Wizara ya Kilimo tunayo Building a Better Tommorow (BBT) ambayo ni kwa ajili ya kilimo biashara. Wizara ya Mifugo na Uvuvi nayo ina programu ambayo ni BBT Life ambayo inahusiana na unenepeshaji mifugo.

Mheshimiwa Spika, hao wote wamekuwa wakikutanishwa na masoko ya ajira lakini pia masoko ya malighafi ambazo wanazitengeneza katika maeneo hayo. Nikiongelea la mwisho ambalo ameniuliza kuhusu changamoto za vigezo na taarifa, hili limeelezwa wazi kwenye mwongozo wa utoaji wa mikopo ya asilimia kumi yaani 4:4:2, almaarufu katika Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, hata sisi kwa upande wa Wizara tumeendelea kufanya hivyo siyo tu katika ufuatiliaji na tathimini lakini pia tumeendelea kutoa elimu kwa vijana na kuitangaza katika maeneo mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko miongoni mwa baadhi ya vijana kwamba hizi programu za mendeleo kwa vijana na hasa zile za kwenda nje zinavyotolewa kunakuwa na upendeleo. Sijui Serikali inasemaje kuhusu tatizo hilo ambalo linalalamikiwa sana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakuhakikishia kwamba Serikali hii haina upendeleo kabisa. Serikali ya Awamu ya Sita imeweka wazi vigezo vya vijana kuweza kupata fursa hizi. Tumekuwa tukizitangaza kwenye vyombo vya habari, tumekuwa pia tukiwaambia Waheshimiwa Wabunge fursa zilizopo. Kuhusu fursa za kwenda nje, tumeingia katika billeteral agreement, na mikataba ya kuhusiana na namna gani vijana wanaweza kupata fursa za ajira tulishaieleza.

Mheshimiwa Spika, wapo Mawakala wa Ajira za nje ya nchi ambao wamesajiliwa chini ya Ofisi ya Kamishna wa Kazi. Pia kupitia TaESA pamoja na SUGECO tumekuwa tukitafuta wahitimu wanaofanya vizuri kwenye vyuo vyote vikuu ikiwemo Chuo cha Kilimo (SUA). Wanafunzi ambao wanafanya vizuri kwenye maeneo mbalimbali wanapata fursa za kwenda kufanya masomo nje ya nchi kwa mfano nchini Israel. Sasa hivi wataenda vijana takriban 600 katika programu hizo.

Mheshimiwa Spika, tunachagua vijana ambao wamefanya vizuri na reccomendation hii inafanywa kwa usaili kwa kupitia Chuo Kikuu chenyewe na kuangalia yale matokeo ya nani amefanya vizuri. Kwa hiyo, hakuna Mtanzania ambaye anazuiwa kufanya vizuri na yeyote anayefanya vizuri anachukuliwa na Serikali kwa ajili ya kwenda kupata masomo hayo nje ikiwa ni sambamba na kupata fursa mbalimbali kulingana na sifa na vigezo ambavyo vimewekwa kwa mujibu wa sheria bila upendeleo, ahsante.
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, nachukua nafasi hii kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya kwa vijana nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; je, Wizara mnampango gani au mnafanya utafiti kuona mafunzo haya jinsi gani yanawanufaisha vijana hao mara baada ya kumaliza mafunzo hayo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; nataka kujua kama Wizara mnamkakati gani sasa wa kuweza kuwaongezea au kuwapa mitaji mikubwa zaidi kwa vile vikundi ambavyo vinafanya vizuri zaidi ili kuweza kuzalisha bora zaidi na kuzalisha vitu vizuri zaidi ili kuendelea kujiajiri na kuajiriwa ili kuweza kuongeza mapato kwa nchi yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Latifa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tunao mpango wa ufuatiliaji na tathmini ambao kila baada ya miezi mitatu tunafanya kupita kwenye maeneo ambayo vijana hawa wapo wakipata mafunzo lakini pia wale ambao wanapewa mitaji mbalimbali. Tumekuwa na utaratibu wa kufanya ufuatiliaji na tathmini ili kubaini na kuona kama kuna tija katika fedha ya nyingi ya Serikali ambayo inatolewa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuweza kuwawezesha vijana kujikimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye hatua ya pili ambapo ameniuliza swali kama tunawapa mitaji? Ni kweli kwamba vijana hawa hatuwaachi tu kwa maana ya kuwatambua na kuwapeleka kwenye maeneo yao ya kupata mafunzo na wanapomaliza kupata mafunzo tunawaunganisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo ambao tunawapeleka VETA, wapo amabao tunawaunganisha kama wamefuzu vizuri kwenda kwenye maeneo ya ajira. Lakini pia tunwaratibu na kuwasaidia kuweza kupata ile mikopo ya 10% ya halmashauri ambapo mwongozo kwa sasa nikijibu swali la kwamba tuwape mitaji inayojitosheleza, tilikua tunatoa kwa vikundi vya watu 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hatua ya sasa na kwa Mwongozo mpya na kwa usikivu wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa vijana aliona ni vema aweze kubadilisha badala ya kuwapa vijana 10, sasa tunatoa mkopo kwa kuanzia shilingi milioni moja mpaka shilingi milioni 10 tumetoka sasa shilingi milioni 10 mpaka shilingi milioni 50 kwa kijana mmoja mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hatua nyingine tunawasaidia pia kuweza kupata mikopo kupitia benki. Zipo benki ambazo zimekwisha kuanza kuonesha mfano. Benki a Azania inatoa mikopo kwa single digit kwa sasa lakini zaidi ya hapo pia tunayo mifuko mingine, katika Wizara ya Kilimo tunao Mfuko wa Pembejeo za Kilimo ambapo vijana hawa nao pia wakimaliza kwenye mafunzo mbalimbali iwe VETA au kule kwenye programu za unenepeshaji ng’ombe au BBT tunawaendeleza kwenda mbali zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni ninayo furaha kukwambia tumepeleka vijana tena awamu nyigine ambao watafikia sasa 700 wanaoenda kupata mafunzo nchini Israel ili kuweza kuwatengeneza vijana na kuweza kuhakikisha kwamba kwa kweli wanatumia fursa za kiuchumi na kushiriki ujenzi wa Taifa lao, ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, pia naomba kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu, nina maswali mawili ya nyongeza.

La kwanza, kwa kuwa upo ushahidi kwamba hiki kinachoitwa taarifa kimekuwa kikitumika na kinaendelea kutumika kuwanyima haki Watanzania ambao hata kama walikutwa na tatizo dogo tu, kufanya kazi katika migodi yote mikubwa Tanzania. Serikali ipo tayari kulitolea maelekezo?

Mheshimiwa Spika, la pili, kwa kuwa taarifa hizi ambazo zimeitwa taarifa, naita blacklisting, zinapomkuta Mtanzania zinadumu milele kinyume na Sheria ya Makosa ya Jinai. Mtu anapotuhumiwa anaadhibiwa na baadaye anakuwa Mtanzania huru.

Je, Serikali ipo tayari kutoa maelekezo ili makosa haya yasiwaadhibu Watanzania milele, wasiajiriwe popote pale katika migodi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge Kanyasu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza la kuhusiana na kwamba anao ushahidi wa matendo haya kutokea. Namuomba Mheshimiwa Mbunge Constantine Kanyasu, anipatie ushahidi huo kama tulivyoahidi kwenye majibu yangu ya msingi ili tuweze kuhakikisha haki za Watanzania hawa zinatendeka kwa sababu, Serikali ni wajibu wetu kulinda pande zote na sisi ndiyo wasimamizi na custodian wa sheria lakini pia usimamizi wa Haki za Binadamu.

Mheshimiwa Spika, ni kinyume kama kweli itakapoonekana ushahidi upo, unaothibitisha kwamba hao watu wametendewa kinyume na kutumia arbitrariness procedures ambazo na pengine wakati mwingine discretional powers ambazo waajiri wao wanakuwa wanazitumia kuwagandamiza Watanzania. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge, nipate orodha hiyo, na mimi na yeye tutafanya kazi hiyo na ninamuahidi tutafika kwenye mgodi husika ambao ameulalamikia.

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu kosa kuwa milele. Ni principle yetu kwamba mtu atatuhumiwa lakini pia utaratibu utafanyika wa kuthibitisha kosa hilo. Kama ni la jinai, itakuwa beyond reasonable doubt na kama ni kosa la dawa, itakuwa ni on balance of probability. Sasa yale ambayo yamethibitika beyond reasonable doubt na hatua zikachukuliwa, maana yake ukishatoa adhabu, haihesabu tena kosa hilo kuja kutumika.

Mheshimiwa Spika, ni kosa kisheria kufanya hivyo, hilo nalo pia ninalichukua na nampongeza Mheshimiwa Mbunge kama amebaini hayo ili tuwatendee haki Watanzania ambao lazima washiriki katika ujenzi wa Taifa lao na kufanya kazi kwa ajili ya nchi hii, ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, kwa nini Serikali isiweke mfumo kwa wastaafu na ukajulikana kabisa kulikoni kusumbuliwa kuleta barua kila wakati wanapodai madai yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali tayari imekwishakuweka utaratibu kupitia mifuko ya pensheni. Sasa hivi hakuna hitaji la kwamba apeleke taarifa zake, tayari tumeshaweka utaratibu ambao moja kwa moja mtumishi anapoelekea kwenye kustaafu miezi sita kabla taarifa zake zinaanza kuandaliwa na sasa tunatoa pensheni yake ndani ya siku 60 na kama hakuna dosari yoyote hata siku tatu anapata mafao yake. Kwa hiyo, changamoto hiyo tumekwishaitatua.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Serikali ndiyo msimamizi mkuu wa mwananchi wa kawaida, hauoni kwamba kuna haja sasa ya Serikali kutoa tamko kwa wamiliki wa magari haya ya IT kwa kuwa wao wanapoingia mikataba wanawadhulumu hawa madereva. Sasa Serikali itoe tamko kuhakikisha wanafuata kile ulichosema cha kima cha chini ili na wao wapate mikataba halali ya kuweza kuendesha magari hayo na kupata ujira unao stahiki badala ya kilometa 900 kulipwa shilingi 100,000? Swali la kwanza hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa utaratibu unaonesha deriva wa IT aruhusiwi kuwa na msaidizi, tukumbuke kwamba magari haya yanaenda kilomita nyingi sana kwa mfano toka Dar es salaam mpaka Tunduma ni zaidi ya kilometa 900 hakuna haja sasa ya Serikali kuruhusu madereva hawa wawe na wasaidizi ili wapunguze ajali? Kwa sababu mara nyingi magari yao yanadondoka njiani kwa uchovu wa madereva kwa kuwa mtu mmoja peke yake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hebron Mwakagenda, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusiana na suala la hawa madereva wa IT kuwasimamia na kuratibiwa na Serikali tayari tunayo Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, lakini pia tunayo sheria kwa makubaliano wanayoyafanya mara nyingi wanafanya makubaliano kwa njia ya mdomo. Tumekuwa tukishauri kwa wakati wote kwamba waingie makubaliano kwa maandishi na sababu ya msingi ni kwamba hizo siyo ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu utoaji wa gari ni wa mtu binafsi au kampuni labda anaagiza gari kutoka Japan linapopitia Bandari ya Dar es Salaam kuipeleka nje ya nchi. Kwa hiyo inakuwa ni kazi ya siku moja au ya wakati tu ambapo dereva atakuwa amefikisha gari hiyo kwenye eneo husika, lakini hata hivyo tumekuwa tukizingatia kwamba katika kipindi cha kufanya kazi hiyo azingatie sheria ambayo ya mkataba ambao ni Sura Namba 345 inayo elekeza maslahi ya watu kwanza wanaoingia kwenye mkataba maslahi, lakini pili kuangalia uzito wa kazi yenyewe husika na ikiongozwa na hili amri ya ajira ambayo ya mishahara hii ambayo tumeitoa ya kima cha chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tutaendelea kusimami hivyo, lakini kwa wale ambao wanafanyakazi kwenye makampuni tumekuwa tukisisitiza wakati wote kuweza kuhakikisha wanakuwa na mikataba ya kazi ili kulinda haki hizo zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili amelieleza kuhusiana na hao madereva wa IT kwa nini hawarusiwi kuwa na msaidizi ndani ya gari? Kwenye hili nitalichukua kwa sababu linahusiana pia na Wizara ya Mambo ya Ndani ili kuhakikisha kweli hawa watu wanakuwa na usalama, lakini pia kuongeza usalama kwa watumiaji wa vyombo vya moto katika barabara. Kwa hiyo, talichukua kwa ajili na nanii nishukuru kwamba ni pendekezo zuri tutalizingatia, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa Jiji la Dar es Salaam linauhitaji sana wa bidhaa za mbogamboga, je Serikali iko tayari kuwasaidia vijana wa Jimbo la Ilala kwa Mheshimiwa Bonnah kuwa na kitu kinaitwa urban farming na hivyo kuwawezesha kulima mazao ya mbogamboga ili kuliwezesha Jiji la Dar es Salaam kujitosheleza kwa bidhaa hiyo na wao kujipatia kipato?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa mazingira ya Dar es Salaam hayafanani sana na Jimbo la Mafinga Mjini. Je, Wizara na Serikali iko tayari kuwasaidia vijana wa Jimbo la Mafinga kuwapa mafunzo mahususi kwa ajili ya kutengeneza bidhaa za mazao ya misitu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bonnah Kamoli yaliyoulizwa na Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, kama Serikali tuko tayari kuweza kuwasaidia vijana waweze kuona kwa kushirikiana na Halmashauri tutaangalia kama suala la urban farming linawezekana kulingana na upatikanaji wa eneo kwenye hilo eneo, lakini pia Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ilishaagiza kila Halmashauri iweze kutenga maeneo kwa ajili ya vijana kufanya kilimo. Kwa hiyo tutaliangalia hilo na tunalizingatia ili kuweza kuhakikisha ombi hilo tunaenda kulitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, lakini kabla ya hilo kuna program pia ya Vitalu Nyumba ambayo tumekuwa tukiitekeleza katika Halmashauri zote nchini zaidi ya 180. Tutaangalia na kuweza kuhakiki kama lot ya pili pia tutazidi kwenda kutoa vifaa na mafunzo ili waweze kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ambalo ameliuliza Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na Mafinga. Kwa sura ileile hili tumelichukua na tutalizingatia, tutashirikiana na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kuona tunatengeneza mazingira mazuri ya vijana wetu kupata ajira,, ahsante.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri yanayoridhisha.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza; je, Serikali imejipangaje kuhusu kulipa mafao ya wastaafu ambao hawajapata mafao hayo nikitolea mfano Wafanyakazi wa Shirika la Ndege Tanzania?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; je, ni hatua gani mnachukua kwa waajiri ambao hawalipi michango ya wanachama kwa wakati? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Malembeka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na malipo au ucheleweshaji wa mafao tayari kwenye hatua hiyo tumeshavuka. Mpaka sasa mifuko yetu PSSSF pamoja na NSSF tayari tumekwishakuanza utaratibu wa ulipaji kupitia mfumo wa teknolojia ya TEHAMA ambapo wanachama wote wanapewa hata taarifa sasa kupitia simu za mkononi au simu ya kiganjani na yeyote yule ambaye amekuwa amecheleweshewa kupata mafao yake tumekuwa tukichukua hatua hasa katika kuhakikisha kwamba tunapata nyaraka zao sahihi na kwa wakati ili waweze kuweza kulipwa.

Kwa hiyo, wachache sana ambao wanapata changamoto hizo kwa sasa na ikitokea changamoto hizo zinatokea tumekuwa tukiwaomba aidha kupitia Mheshimiwa Waziri ambaye alizunguka Mikoa karibia nchi nzima kwa kupitia kikanda kwenye majiji alikutana na wastaafu na tumekuwa tukipokea na tuna desk maalum la kupokea changamoto hizo. Kwa hiyo, kama zipo nimuombe Mheshimiwa Mbunge anifikishie ikiwa ni pamoja na za ATCL kwa taarifa tulizonazo ofisini tayari wapo walikwishakulipwa zaidi ya wafanyakazi 500 na wale wachache ambao walikuwa wana changamoto ilikuwa ni kuhusiana na taarifa sahihi hazikuweza kuwasilishwa ofisini ili waweze kulipwa. Kama watakuwa wamepata nyaraka na taarifa sahihi tuko tayari kuweza kuwalipa mafao yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili la waajiri kutokuwasilisha michango kwa wakati. Mifuko hii inazo sheria ambayo inaianzisha na katika sheria hizi zinaeleza ni kosa kwa mwajiri kutokuwasilisha michango kwa wakati katika mifuko hii kwa ajili ya wanachama na ikitokea hivyo hata mahakamani Bunge lako tukufu lilitunga sheria hii kwa kujua umuhimu wa watu hawa ni katika mfumo wa summary suit. Kwa hiyo, unapelekwa mahakamani, hakuna kujitetea na tunachua hatua.

Kwa hiyo, kama kuna maeneo ambayo watakuwa wamechelewesha michango kwa kweli nitoe rai kupitia Bunge lako tukufu kwamba tunawataka waajiri wote nchini kutekeleza hilo, kupeleka michango kwa wakati ya wanachama ili wasisumbuke, lakini pia sisi pia kutupunguzia mashauri yaliopo mahakamani, mpaka sasa tuna mashauri zaidi ya 26 na tumechukua hatua, ahsante.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante; kwa kuwa suala la wastaafu kama hilo liko sawasawa na walioko Zanzibar, je, Wizara yako inatoa faraja gani kwa wale walioko Zanzibar wanaokawia kupata mafao yao au hawapati kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shomar kama alivyoeleza kuhusiana na kwamba changamoto zilizo upande wa Bara ni sawa na zile zilizopo upande wa Zanzibar. Kwa kuwa hii ni Serikali ya Muungano na tunafanyakazi kwa collective responsibility ninaomba kulichukua swali hili na tutawasiliana na Mamlaka za Zanzibar ili kuhakikisha wastaafu wetu hawapati tabu baada ya kustaafu.

Mheshimiwa Spika, pia nilieleze Bunge lako tukufu kwamba nimechukua na kupokea mwongozo wako kuhusiana na changamoto ambazo wanazipata. Lakini pia nitumie nafasi hii kwa sababu tumeshachukua hatua sana kuhusiana na kuwapeleka mahakamani, wakati mwingine mashauri pengine yanachelewa na watu wetu wanazidi kuumia.

Sasa naomba nifanye hatua moja na kwa Mheshimiwa Waziri kama hatua tuliokwishakuichukua kama unaniruhusu nitaje namba ya simu ambayo wakituma ujumbe pale mara moja wanaweza kupata huduma, lakini pia tuna ma–desk yetu kwenye zile ofisi tumezi–establish sasa kwa ajili ya kuwapa huduma wastaafu wetu na ni kwa kupiga simu tu ama kwa kuwasiliana kupitia WhatsApp na tunachukua hatua hizi.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tukifanya mzaha wa hawa wastaafu na changamoto ambazo zimekuwepo tutachukua hatua kwa mameneja wetu wa mikoa ili kama hawezi kuwahudumuia Watanzania basi waje wengine wanaoweza kuwahudumia na hili ni agizo langu kwa mikoa yote wahakikishe hakuna malalamiko ya wastaafu na mameneja tutawapima kwa kiwango cha wanaolalamika kuhusu wastaafu. (Makofi)

SPIKA: Haya watajie namba maana ikitajwa hapa itakuwa na uzito, watajie namba wastaafu.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, namba ni 0715939902. Ni 0715 939902, ahsante.
MHE. TAMIMA HAJI ABASS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, Serikali imejipangaje kutoa uelewa kwa watumishi wanaotarajia kustaafu hasa kuhusu kikokotoo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tamima kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumeendelea kutoa elimu ya kuhusiana na kikokotoo na kwa msingi huo mifuko yetu imeshirikiana na Chama cha Waajiri (ATE) katika kutoa elimu, lakini pia Shirikisho la Wafanyakazi (TUCTA), lakini pia tumekuwa tukiwafikia hata kwenye makundi kulingana na kada zilizopo za ajira. Kwa hiyo, hata hao ambao ameeleza Mheshimiwa Mbunge tutawafikia na swali la utoaji wa elimu kuhusiana na kikokotoo ni endelevu ili waweze kuona faida ambayo wanaweza kuipata kutokana na kikokotoo hiki kipya, ahsante.

MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wastaafu wengi wamekuwa wanapata adha ya kufanya uhakiki wa mara kwa mara kuthibitisha kwamba bado wako hai, proof of life na wanahitajika kwenda makao makuu ya Wilaya au ama katika taasisi ambazo walistaafu kwa ajili ya kwenda kufanya hiyo proof of life?

Je, ni mkakati gani ambao Serikali mtachukua kuhakikisha kwamba kunakuwa na mfumo wa kisasa wa kuweza kufanya hiyo proof of life badala ya usumbufu ambao unaendelea kwa hivi sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndugulile kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kulikuwa na changamoto sana ya wastaafu wetu kwenda kuambiwa kwamba anaenda kuhakikiwa taarifa na kadhalika, lakini tuliliona hilo na tukaanzisha mfumo maalum wa kuwahitaji wao kuwa na namba zao za mawasiliano za kiganjani, lakini pia kuanzisha portal maalum ya kutoa taarifa za wanachama na hatua ya pili tuliyoichukua ni kwamba kuhakikisha sasa taarifa hizi zinaenda on monthly basis kuhakikisha kwamba taarifa zake kwa wakati wote zinapatikana kwa Mfumo wa TEHAMA. Kwa hiyo, tumejihimarisha kwenye TEHAMA na tunafanya vizuri na sasa tumekwishakuanza kuwahudumia vizuri, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa wapo walimu ambao michango yao ilikuwa haikupelekwa na watumishi, lakini wakaambiwa wajilipie wenyewe, wamejilipia wenyewe, wana risiti mkononi, lakini marekebisho ya mafao yao hayakufanyika.

Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na walimu hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Kisangi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kwa Mwanachama ambaye alikuwa amesajiliwa kihalali na sahihi kabisa, lakini pia kuna mwajiri ambaye alikuwa na wajibu wa kulipa michango hajatekeleza wajibu wake na badala yake mwanachama akalazimika kujichangia mwenyewe, hilo kwanza siyo sahihi na linahitaji ufuatiliaji.

Kwa hiyo, niombe nipate takwimu sahihi za wanachama hao ambao walifanya hivyo na bado pia hawajaweza kutendewa haki, tulichukue kama ofisi na kwenda kulifanyia kazi, kwa sababu sina takwimu sahihi nitaomba nipate majina lakini pia na takwimu zao ili niende nikafanye ushughulikiaji wa jambo hili, ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, madai ya watumishi wa kilichokuwa Kiwanda cha Sukari Kilombero na process nzima ya ubinafsishaji limebaki kuwa kovu kwenye kidonda kwa wananchi hawa.

Swali langu kwa Serikali; kuna mkataba wa hiari kati ya watumishi hawa na kilichokuwa Kiwanda cha Sukari Kilombero ambao haujatekelezwa mpaka sasa; je, nini hatua za Serikali katika utekelezaji wa hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuna kauli ya Serikali ambayo ilitolewa na Waziri Kusila pamoja na Waziri Kimiti walipokutana na watumishi hawa mwaka 2000.

Nini utekelezaji wake ili kutibu majeraha ambayo yametokana na ubinafsishaji wa kiwanda hiki cha sukari?

SPIKA: Mheshimiwa Londo, hilo la pili Mheshimiwa Naibu Waziri anajua kweli ama unazo hizo taarifa hapa?

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, suala hili lipo katika Ofisi ya Waziri Mkuu.

SPIKA: Hilo ni la nyongeza.

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, ni la nyongeza, ndiyo.

SPIKA: Ndiyo, sasa ili yeye aweze kuwa na majibu lazima ajue hao wawili uliowataja walisema nini, ndiyo nauliza Mheshimiwa Waziri hizo taarifa za walichosema anazo? Maana swali lako ni la msingi, lakini sasa nataka kujua yeye anayo? Maana asije akatupa majibu ambayo wale hawakusema.

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, Serikali iliahidi kuwapatia mshahara wa miezi kumi kati ya 40 ambayo ilikuwa ni kifuta jasho kwa watumishi hawa. Sasa utekelezaji mpaka leo hawajatekeleza, nini kauli ya Serikali.

SPIKA: Ahaa, kwa hiyo hicho ndicho walischosema hao wawili?

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, ndiyo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Jimbo la Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kuhusiana na mkataba wa hiari aliousema, unaitwa mkataba wa hali bora kwa mujibu wa sheria. Katika mkataba huu wa hiari, bado ni sawa na mikataba mingine kwa mujibu wa Sheria yetu ya Mikataba Cap. 345, na kama kutakuwa kuna utekelezaji ambao haukufanyika, hilo ni eneo la kwenda kufuatilia na kuweza kushughulikia.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, mtakumbuka kwamba katika kesi hii ilikuwa ni suala ambalo lilihitaji majadiliano katika upande wa wafanyakazi, Chama cha Waajiri, lakini pia uongozi wa kiwanda wakati wanabinafsisha kiwanda hicho. Na katika kipindi hicho mbali na yale ambayo yalizungumzwa kama utatuzi ya mgogoro, kulikuwa kuna mashauri ambayo yalikwenda mahakamani, sasa katika mashauri yaliyokwenda mahakamani kuna uamuzi wa mahakama ambao ulifanyika, kama malipo yatakuwa hayajafanyika, utaratibu wa kisheria ni kufanya execution of decree. Kwa hiyo enforcement of the execution of decree kama haikufanyika, nitawasiliana na Mheshimiwa Mbunge tuweze kuona, kwa sababu mahakama ilifanya maamuzi mahususi, niwasiliane naye, na kama kesi hiyo itakuwa kubwa kwa kiwango chake tutaona namna ya kwenda kushirikiana na kukutana na wafanyakazi hao ili haki yao iweze kupatikana kwa mujibu wa sheria na maamuzi ya mahakama, ahsante.
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hili tatizo la ajira ni tatizo kubwa sana hapa nchini hivi sasa. Je, kwanini Serikali isifanye tracer study na kuandaa database ya vijana wote wanaohitimu mafunzo ili kuweza kuwatambua, kuweza kuwafuatilia na kujua namna nzuri ya kuwapatia ajira Serikalini pamoja na sekta binafsi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwanini Serikali isiandae mfumo mzuri wa kuwakopesha hawa vijana, wale wanaotaka kuingia kwenye ujasiriamali hata walau mtaji wa Milioni 20 wa kuanzia na wakajidhamini kwa vyeti vyao vya vyuo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mweyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwa na tatizo la ajira lakini kwa sehemu kubwa Serikali imeweza kulifanyia kazi Serikali ya Awamu Sita ya Mama Samia Suluhu Hassan. Tumekuwa na mikakati mingi ya kuweza kuhakikisha tatizo hili linapungua, mojawapo kwanza amefungua private sector kwa kubadilisha sheria pamoja na sera. Sambamba na hilo katika maeneo mengi vijana sasa wameanza kupata ajira kwenye miradi mikuwa ya maendeleo, lakini sambamba na hilo wameendelea kutoa ajira katika Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili katika kutafuta kanzidata, ni kweli tumekuwa katika kila nafasi ambazo zinatolewa kwa ajili ya ajira majina yale ambayo wamekuwa waombaji tumekuwa tukiyachukua kupitia kitengo cha ajira TAESA ili kuweza kupata takwimu sahihi za vijana ambao wamemaliza Vyuo Vikuu. Sambamba na hilo hatuwaachi hivyo, kumekuwa na mafuzo mbalimbali ya kuwapa internship, wapo vijana ambao wamepelekwa TRA na taasisi nyingine nyingi za Serikali kuweza kupata mafunzo ya uzoefu kazini sambamba na kuanzisha pia utaratibu wa kuwauhisha wale ambao wamehitimu kwenye vyuo mbalimbali vikiwemo vya VETA na FDC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo hilo tumekwishakuanza kufanya, tumemaliza manpower survey kuweza kujua, lakini tunaenda kwenye hatua mbili sasa ya kufanya labour survey kuweza kujua idadi ya vijana ambao wanaweza kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusiana na mikopo, Serikali hii imekuwa ikitoa mikopo ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan tena kwa upendo mkubwa, ukiangalia hakuna kijana yoyote ambaye hapati mkopo, kumekuwa na scheme za utoaji mikopo katika elimu. Kwa mfano, kwa Shule za Msingi, tumekuwa tukitoa elimu bila malipo, lakini akimaliza sekondari anaenda Chuo Kikuu anakutana na bodi ya mikopo ambayo inampa mikopo, akitoa Chuo Kikuu, anapokuja nje anaenda kwenye Halmashauri zetu tunatoa mikopo ya 4:4:2 kwa maana ya asilimia Nne (4) kwa wanawake, asilimia Nne (4) kwa vijana na asilimia Mbili (2) kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo tumekuwa na scheme nyingine za makubaliano na mabenki mbalimbali kuweza kushusha riba na kutoa mikopo ikiwemo benki hizo za kilimo ambazo tayari zimekwishaanza kutoa na yalikuwa ni maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuweza kuhakikisha katika kila Halmashauri wanatenga maeneo maalum ya vijana kwa ajili ya kufanya kilimo na wanapewa mikopo kupitia Benki lakini pia Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge pia Mheshimiwa Luhanga Mpina ambaye ndiye muuliza swali kama mtapitisha bajeti ya Wizara ya Kilimo, kule kuna mpango wa building the better tomorrow ambao unaenda kugusa vijana zaidi ya Milioni Moja katika kuhakikisha wanatengenezewa scheme za maeneo ya kilimo kwa maana ya block farming na wajibu wa Wizara ya Kilimo, itakuwa ni kuandaa kwanza maeneo hayo lakini pili kutafuta fecha kwa ajili ya kuwapa vijana hao na kuweka miundombinu na tatu ofisi ya Waziri Mkuu itakuwa wajibu wa kuweza kuratibu shughuli hizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa hayo tumeyaona kwa kweli vijana wakae tu mkao wa kula na watoe ushirikiano kwa Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan inawaona na inawaangazia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan hivi juzi, ametoa zaidi ya Shilingi Milioni 10 kila Mkoa kwa ajili ya wamachinga. Kwa hiyo, vijana wengi wako kwenye eneo hilo, ahsante. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko dhamira ya Serikali ya kutoa ajira kwa vijana hasa kupitia vitalu nyumba, lakini vitalu nyumba hivi ni ghali sana. Je, Serikali iko tayari sasa kuweka ruzuku katika vitalu nyumba ili vijana wengi waweze kujiajiri kupitia eneo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Massare, kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumekuwa na programu ya kutoa elimu kwa ajili ya vijana kujifunza utengenezaji wa vitalu nyumba na tumekwishakufanya katika Halmashauri zaidi ya 82 na katika hayo maeneo ilikuwa wajibu wa kwanza ni kuhakikisha kwamba elimu inatolewa, lakini pia fedha na gharama zote zinaratibiwa na Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan kupitia ofisi ya Waziri Mkuu. Ni kweli kitalu nyumba kimoja kilikuwa kinagharimu zaidi ya karibia shilingi milioni 12, baada ya kuliona hilo na kwa ushauri mzuri wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria na muuliza swali Mheshimiwa Massare akiwa mjumbe tulitembelea Zanzibar na tuliweza kuona kwamba kuna uwezekano wa kutengeneza vitalu nyumba bila kutumia mabomba ya chuma na kutumia tu vitu vya asili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumekwishakuanza kuwa-engage wataalam kuweza kutusaidia zaidi namna gani watashusha gharama na kutafuta wadau wengine ambao watasaidia katika kuweza kuwapa mikopo vijana hawa katika maeneo haya. Kwa kweli eneo hili limeonekana linapokelewa vizuri na vijana, tutahakikisha kwamba kwa ushirikiano na ushauri ambao mnautoa tutaufanyia kazi kila wakati. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi ambavyo unaeleza ni kama vile uko nje ya Tanzania. Tuna vijana wengi sana wamekosa ajira zaidi ya miaka sita sasa, lakini unasema kule chini kuna nafasi kwenye Halmashauri za wao kupata fedha, ninafahamu kuna ile 4.4.2 kama ulivyosema, lakini mwisho wa siku vijana wengi mfumo unawaacha nje kwa sababu hawana sifa za kupata mikopo hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakagenda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wako vijana wengi ambao kwa wakati huo na kwa jinsi alivyosema ameshindwa kutueleza takwimu hasa, Serikali tunazo takwimu za vijana hawa, tumeshafanya Manpower survey, lakini wale wote wanaofanya application ya ajira, Vyuo Vikuu vyote tumekuwa tukipata taarifa za ajira na demographic population ya wanafunzi ambao wanamaliza Vyuo Vikuu at least kila mwaka. Tunao vijana zaidi ya Laki Mbili wanaoingia kwenye soko la ajira kutoka vyuo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya takwimu nikuambie Mheshimiwa ninazo za kutosha hapa na tutakueleza Serikali inawajali vijana kwa kiwango gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tunayo mifumo na programu ambazo tunaziandaa, labda programu ya kwanza nikikupa tu kwa faida yako tu Mheshimiwa uweze kujua na mengine nitakushirikisha ili tuwasaidie vijana kwenye eneo ni pamoja na hiyo internship ambayo inatusaidie siyo tu katika kuwafanya kupata mafunzo kazini, pia inawasaidia vijana hawa kuweza kuangaliziwa ajira ndani ya nje ya nchi kupitia wakala mbalimbali wa ajira waliosajiliwa na Ofisi Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo pia tumekuwa tukiendelea kuhakikisha tunatoa mikopo. Kwa hiyo, takwimu zipo, zaidi ya bilioni 150 zimekwishatolewa kwa vijana mbalimbali. Kwa hiyo, kama kuna vijana ambao wapo, labda pengine siyo Watanzania ni Wakenya, utanisaidia ili niweze kuwaingiza hapa na kuweza kuona ni namna gani tunawasaidia. Kwa hiyo, ninakutaarifu tu kwamba nipo Tanzania na huu ndiyo utaratibu wa Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan, Serikali ya takwimu na utekelezaji na Serikali inayowapenda vijana. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali kuhusiana na wastaafu kulipwa mafao kwa wakati, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko ya kuchelewa kulipwa mafao yao mapema na malalamiko makubwa yamekuwa kwamba kuna baadhi ya wastaafu makato yao yanakuwa hayajapelekwa kwenye mifuko hiyo. Nini kauli ya Serikali kwenye eneo hili kwa sababu limekuwa na usumbufu mkubwa ambao hauna sababu kwa sababu wamekuwepo kwenye utumishi kwa miaka yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wastaafu wamekuwa wakiombwa taarifa zao upya baada ya kuwa wameshastaafu. Serikali inakuwa ina taarifa zao zaidi ya miaka 30 haioni kwamba ni usumbufu wa kuwaomba wastaafu ambao wamekuwa nao kwa miaka yote ya umri wao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusiana na malalamiko ya ucheleweshaji wa malipo tayari tumekwishakufanyia kazi, unakumbuka katika Bunge lako hili yalitolewa maelezo mahsusi na Waziri mwenye dhamana, wakati huo Mheshimiwa Mhagama, na sasa Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, tumekwishakuanza kufanya tathmini na mapitio upya kuweza kuhakikisha kwamba wanalipwa kwa wakati na tayari kuna mifumo mbalimbali ya kitehama ambayo imeanzishwa, ikiwemo mfumo wa MAS pamoja na CFM, hii yote ni kwa ajili ya kutengeneza ile membership administration system ambayo ni mfumo wa ki-TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo hivi karibuni tutaanza ziara ya mkoa kwa mkoa kuweza kuanza kusikiliza changamoto za wastaafu ikiwa ni pamoja na kuhakiki taarifa mbalimbali ili kuweza kuhakikisha kwamba wanalipwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la pili, ameulizia kuhusiana na hawa wastaafu wanapoombwa taarifa mpya. Utakumbuka kwenye Bunge lako hili tulitoa taarifa kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba hili suala la uombaji wa barua za wastaafu limefikia mwisho, kwa sababu taarifa hizi sasa ni wajibu wa mifuko yenyewe kuweza kuhakikisha zinatunza kumbukumbu sahihi za wanachama wake ikiwa ni pamoja na ndani ya huo mfumo wa membership administration service system, pamoja na mfumo wa NSSF weyewe ambao ni core fund management system zote hizi taarifa zitakuwa mle.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaendelea kutumia fursa hii kuwasihi waajiri kote nchini kuwasilisha michango kwa wakati ya wanachama ili wasihangaike. Pili kuhakikisha mfuko wenyewe unahakiki taarifa za wale wastaafu hata mwaka mmoja kabla ya kustaafu ili kupunguza usumbufu kwa watumishi hawa waliotumikia Taifa vizuri. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Wafanyakazi wa TAZARA wamekuwa wakiidai Serikali mafao yao na wamechangia michango yao yote katika kipindi cha utumishi wao, TAZARA ilikuwa haipeleki michango kwa wahusika.

Je, Serikali inawasaidia vipi hao wafanyakazi ambao wengi wao wamefariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama alivyokwisha kuuliza kuhusiana na wafanyakazi wa TAZARA ambao wamekuwa na changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tayari jambo hili linaendelea kushughulika nalo lakini kwa nia njema ya dhati kabisa ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan, ilitokana na ile mifuko minne ambayo iliunganishwa. Katika ile mifuko minne ilirithi deni la Shilingi Trilioni 1.02 ya wanachama hawa ambao walikuwa wanadai katika maeneo mbalimbali. Nilitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba nina furaha kwamba fedha hizo zimelipwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan ameongeza pia fedha zaidi ya Trilioni 2.17.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa, kiwanda cha nyuzi Tabora mpaka kinafungwa wafanyakazi wengi walikuwa hajalipwa mafao yao ya kustaafu. Ni lini Mheshimiwa Waziri upo tayari tuiongozane kwenda kuwasikiliza wale wastaafu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwakasaka kama alivyouliza kuhusiana na wastaafu wa kiwanda hicho cha Tabora, nipo tayari kumpa ushirikiano kuwasikiliza, pia Serikali itatoa fursa hiyo kuweza kuhakikisha kwamba haki zao hazipotei. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Mheshimiwa Ikupa, napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sheria hiyo Na. 9 ya mwaka 2010 ndiyo sheria pekee ambayo inaonesha haki zote za watu wenye ulemavu; na kwa kuwa marekebisho ya sheria hiyo yanategemea marekebisho ya sera: Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha inaharakisha mchakato huo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa watu wenye ulemavu wana haki nyingi sana za kimsingi na wapo wengi ambao hawaelewi haki zao za kimsingi ikiwepo upatikanaji wa ajira, elimu na mambo mengine: Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutoa elimu kwa watu wenye ulemavu ili waweze kutambua haki zao na pia kutoa nyongeza katika marekebisho ya sheria hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, tumeshaanza kufanya kazi ya kufanya mapitio ya Sera ya Watu Wenye Ulemavu kwa sababu sera hiyo ni ya mwaka 2004 na sheria ni ya mwaka 2010. Kwa hiyo, katika kufanya hivyo, sera ndiyo inayotangulia ili iweze kutengeneza mazingira mazuri zaidi na kufanya tathmini na kuwashirikisha wadau wote ili kuweza kujua changamoto za sasa zinazowakumba watu wenye ulemavu ili kuweza kuwahudumia vizuri zaidi na kutunga sheria ambayo itakuwa inaendana na mahitaji halisia katika mazingira yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tayari tumeanza kwa mwaka huu wa fedha 2023/2024. Matarajio yetu, tutakuwa tumemaliza kwenye hatua ya sera, na 2024/2025 tutakuwa tunaenda sasa kwenye kutunga sheria ambapo tayari hatua ya awali tumeshaanza na procedure ya kufanya mabadiliko kwenye sera, kukutanisha wadau, kufanya situational analysis kwenye mikoa na maeneo mbalimbali, na pia kukutanisha mashirikisho ikiwemo Shirikisho la Chama cha Watu Wenye Ulemavu na Shirikisho la Wanawake Wenye Ulemavu na taasisi nyingine zote ambazo zinahusika na haki za watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama nilivyoeleza, ndani ya mwaka huu wa fedha tutakuwa tumejitahidi kwenye upande wa sera na mwaka wa fedha unaofuata tutakuwa tumeumaliza katika upande wa kutunga sheria ambapo itakuwa muafaka wa kutibu changamoto ambazo zinawakumba watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ameniuliza kuhusiana na haki za msingi za watu wenye ulemavu kwamba wapo wengi ambao hawazifahamu. Tumeendelea kufanya hivyo, mbali na kuwa na sera na sheria ya watu wenye ulemavu, tumekuwa tunasajili pia taasisi mbalimbali ambazo zinaendelea kutoa elimu na kusimamia haki za watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, upande wa Serikali pia tumeendelea kutoa elimu kupitia vyombo vya habari lakini pia kuyafikia makundi mbalimbali ikiwemo kuunda mabaraza ya kuanzia ngazi ya kata mpaka Taifa ya watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na kushirikiana na mashirikisho ya watu wenye ulemavu ili kuendelea kutoa elimu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanya hivyo pia, alitoa fedha zaidi ya shilingi bilioni tatu kufufua vyuo zaidi ya saba vya watu wenye ulemavu ambapo tumeshafanya kazi hiyo. Lengo ni kuwapa fursa zaidi watu wenye ulemavu na kuwaingiza waweze kujitegemea. Zaidi tumeboresha hata mwongozo unaotoa haki kwa watu wenye ulemavu kupata mikopo ya asilimia mbili kutoka kundi la watu wenye ulemavu watano na sasa mkopo anaweza kupata mtu mwenye ulemavu mmoja na tunaweza kumpa mkopo wa kuanzia shilingi milioni moja hadi milioni hamsini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jitihada za Serikali zinazofanyika ni kubwa, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, vijana wanatofautiana katika sifa, makundi na mahitaji; je, ni kwa kiasi gani programu hizi zimezingatia changamoto hiyo?

Swali la pili, tumeona katika sekta ya elimu sasa tumekuja na mtaala mpya ambapo mafunzo ya stadi kwa maana ya amali yataanza katika ngazi ya msingi; je, katika hayo maboresho ambayo Serikali inakusudia kuyafanya Serikali iko tayari kuzingatia eneo hili la mtaala mpya wa elimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid Shangazi ambalo kwanza ni kuhusiana na sifa na makundi mbalimbali ya vijana, jinsi ambavyo Serikali imeweka programu za kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali tumeweka programu mbalimbali kulingana na mtawanyiko wa makundi pia mikakati imewekwa kwa ajili ya kuangalia namna gani ambavyo vijana hawa wanaweza kufikiwa wote katika Taifa. Moja ya programu ambazo tumeziweka tumeangalia pia programu kisekta, kwa mfano kwenye sekta ya elimu, vijana walio wengi kama viongozi wa baadaye wa Taifa hili wamewekewa programu na Serikali ya kupewa msaada wa elimu bure au elimu bila malipo mpaka Kidato cha Sita na akimaliza Kidato cha Sita ataenda Chuo Kikuu ambako anakutana na mkopo na sasa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefikisha mkopo wa elimu ya juu kufikia shilingi bilioni 734.

Mheshimiwa Mwenyekiti, programu nyingine ambayo ipo ya kisekta ni kwenye eneo la uchumi, biashara na uwekezaji. Hapo pia tuna Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, sambamba na hilo kwenye Halmashauri zetu tumeweka programu ya utoaji wa mikopo pia fursa za ajira na mitaji. Katika eneo hilo zile asilimia nne zinaenda kwa ajili ya vijana na watu wenye ulemavu lakini pia wanawake, wanasaidiwa hata awe amemaliza Chuo Kikuu au hayupo kwenye sekta ya kisomo anaweza akapata fedha zikamsaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye sekta ya madini, tumeenda kisekta katika Wizara kuangalia, sekta ya madini pia wapo wale wachimbaji wadogo wadogo vijana, nao wanawezeshwa huko kulingana na programu na miongozo ambayo tumeiweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya kilimo pia tuna BBT LIFE ambayo ni Building Better Tommorrow kwa ajili ya kuwasaidia vijana waweze kujifunza namna ya kunenepesha mitamba ya ng’ombe na pia kufanya cage fishing na mafunzo mengine yanayoendana na masuala ya uchumi wa bahari. Zaidi ya hapo kwenye kilimo tuna vijana, tuna BBT LIFE ambayo ni kilimo biashara. Mafunzo yanaendelea na zaidi ya vijana 800 walikuwa wanufaika na programu hizi ni endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sekta nyingine ya ajira na kazi, tuna kitengo maalum cha ajira kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu cha TAESA, ambapo vijana wanaomaliza vyuo vikuu wanaenda kwa ajili ya mafunzo ya utayari kazini. Pia tuna programu za ukuzaji ujuzi, tuna programu za wanagenzi, zote hizi zinalenga kuwagusa vijana kwenye makundi mbalimbali. Zipo pia programu kwenye sekta ya michezo na sekta nyingine kwa sababu ya muda, lakini uone jinsi gani Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imewaangalia vijana katika maeneo yote. Hata wale ambao wana-aspire kwenye uongozi wa Taifa kwenye maeneo ya siasa, vyama vya siasa tumefanya mabadiliko ya Sheria hapa kwamba vijana waangaliwe pia katika kupewa fursa kwenye vyama vyao na kuweza kupata fursa za uongozi. Ahsante. (Makofi)
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, pamoja na majibu ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, fedha iliyokuwa imetengwa ni shilingi bilioni 6.53 lakini mpaka sasa fedha iliyotolewa ni shilingi bilioni 1.14 hasa ukizingatia sasa hivi tuko mwezi wa Nane wa mwaka wa kibajeti bado miezi minne tu ili tuweze kumaliza mwaka wa fedha. Nataka kujua ni mpango upi wa Serikali kuhakikisha mnapeleka fedha zote kwa wakati ndani ya mwaka huu wa bajeti ili chuo hiki kiweze kujengwa kwa wakati?

Swali langu namba mbili, nataka kujua, je, Serikali mna mkakati gani sasa wa kuhakikisha mnapata wakufunzi wa kutosha na wanafunzi ili chuo hiki kitakapoanza kiweze kufunguliwa kwa muda na kuanza kwa wakati, nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI) K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Stella Fiyao, kama alivyouliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ni kweli kwamba kulikuwa na ucheleweshaji kidogo wa upelekaji wa fedha katika fedha ambayo ilikuwa imetengwa ya shilingi bilioni 6.53 lakini mpaka hatua hii ninavyosema shilingi bilioni 1.14 imekwenda na katika mwaka huu wa fedha katika hatua hii ya mwisho tayari kuna fedha zingine ambazo tunatarajia kuzitoa kwenye disbursements nyingine. Changamoto tu ilikuwa ni ya upatikanaji wa fedha lakini azma ya Serikali na dhamira ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassani ya kujenga imeendelea kuwepo na siyo tu kwa Mkoa wa Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge atakumbuka kuwa tunajenga eneo la Mbozi katika Halmashauri ile lakini pia kwenye Mikoa mingine ujenzi unaendelea. Kwa hiyo, usiwe na wasiwasi nafurahia kwamba ana dhamira ya dhati kuona kwamba chuo kile kinaanza kufanya kazi. Kwa hiyo, fedha zitapelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameuliza kama tunao mpango gani kuhusiana na kupeleka wakufunzi pamoja na wanafunzi wa kujifunza pale. Dhamira ya Serikali ya kujenga vyuo hivi katika andiko lake kuu ni pamoja na uwepo wa vitendeakazi, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba wafanyakazi wanakuwepo lakini pia vifaa vya kijifunzia na mashine za wanafunzi hawa kujifunza, yote haya yako katika mpango wa bajeti na kwamba tutaenda kukamilisha mara pale chuo kitakapokamilika ili wanafunzi hawa wa Kitanzania waweze kupata fursa hiyo ya kujifunza na kuchangia katika ujenzi wa Taifa, ahsante. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, vijana wanatofautiana katika sifa, makundi na mahitaji; je, ni kwa kiasi gani programu hizi zimezingatia changamoto hiyo?

Swali la pili, tumeona katika sekta ya elimu sasa tumekuja na mtaala mpya ambapo mafunzo ya stadi kwa maana ya amali yataanza katika ngazi ya msingi; je, katika hayo maboresho ambayo Serikali inakusudia kuyafanya Serikali iko tayari kuzingatia eneo hili la mtaala mpya wa elimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid Shangazi ambalo kwanza ni kuhusiana na sifa na makundi mbalimbali ya vijana, jinsi ambavyo Serikali imeweka programu za kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali tumeweka programu mbalimbali kulingana na mtawanyiko wa makundi pia mikakati imewekwa kwa ajili ya kuangalia namna gani ambavyo vijana hawa wanaweza kufikiwa wote katika Taifa. Moja ya programu ambazo tumeziweka tumeangalia pia programu kisekta, kwa mfano kwenye sekta ya elimu, vijana walio wengi kama viongozi wa baadaye wa Taifa hili wamewekewa programu na Serikali ya kupewa msaada wa elimu bure au elimu bila malipo mpaka Kidato cha Sita na akimaliza Kidato cha Sita ataenda Chuo Kikuu ambako anakutana na mkopo na sasa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefikisha mkopo wa elimu ya juu kufikia shilingi bilioni 734.

Mheshimiwa Mwenyekiti, programu nyingine ambayo ipo ya kisekta ni kwenye eneo la uchumi, biashara na uwekezaji. Hapo pia tuna Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, sambamba na hilo kwenye Halmashauri zetu tumeweka programu ya utoaji wa mikopo pia fursa za ajira na mitaji. Katika eneo hilo zile asilimia nne zinaenda kwa ajili ya vijana na watu wenye ulemavu lakini pia wanawake, wanasaidiwa hata awe amemaliza Chuo Kikuu au hayupo kwenye sekta ya kisomo anaweza akapata fedha zikamsaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye sekta ya madini, tumeenda kisekta katika Wizara kuangalia, sekta ya madini pia wapo wale wachimbaji wadogo wadogo vijana, nao wanawezeshwa huko kulingana na programu na miongozo ambayo tumeiweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya kilimo pia tuna BBT LIFE ambayo ni Building Better Tommorrow kwa ajili ya kuwasaidia vijana waweze kujifunza namna ya kunenepesha mitamba ya ng’ombe na pia kufanya cage fishing na mafunzo mengine yanayoendana na masuala ya uchumi wa bahari. Zaidi ya hapo kwenye kilimo tuna vijana, tuna BBT LIFE ambayo ni kilimo biashara. Mafunzo yanaendelea na zaidi ya vijana 800 walikuwa wanufaika na programu hizi ni endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sekta nyingine ya ajira na kazi, tuna kitengo maalum cha ajira kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu cha TAESA, ambapo vijana wanaomaliza vyuo vikuu wanaenda kwa ajili ya mafunzo ya utayari kazini. Pia tuna programu za ukuzaji ujuzi, tuna programu za wanagenzi, zote hizi zinalenga kuwagusa vijana kwenye makundi mbalimbali. Zipo pia programu kwenye sekta ya michezo na sekta nyingine kwa sababu ya muda, lakini uone jinsi gani Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imewaangalia vijana katika maeneo yote. Hata wale ambao wana-aspire kwenye uongozi wa Taifa kwenye maeneo ya siasa, vyama vya siasa tumefanya mabadiliko ya Sheria hapa kwamba vijana waangaliwe pia katika kupewa fursa kwenye vyama vyao na kuweza kupata fursa za uongozi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Waziri kwa ushirikiano katika eneo hilo nimekuwa nikisaidia sana. Lakini swali langu la kwanza swala la wadau kutoa maoni pamoja na elimu limefanyika kwa muda mrefu sana.

Je, Serikali kupitia comissionar wa kazi haioni iko haja sasa ya kuharakisha kuridhia mkataba huo angalau wawe parcial ili wafanyakazi hao wawe rasmi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, baada ya Serikali kupitia VETA na CVM kuzindua mitaala ya wafanyakazi wa majumbani, je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza udahili wa wanafunzi hao kwa sababu sasa hivi hata wanafunzi kutoka Vyuo Vikuu na Vyuo vingine wanaajiriwa kufanya kazi majumbani. Ni mpango gani sasa Serikali inafanya ili wanafunzi wawe wengi katika hivyo Vyuo vya VETA? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI) Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Thea Medard Ntara kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mkataba huu wa kimataifa tayari Serikali ilikwisha kuanza kuchukua hatua toka mwaka 2021 lakini kwa sehemu kubwa kama Mheshimiwa Mbunge anavyoelewa na nampongeza sana amekuwa akipambana sana amekuwa akipambana sana kuhusiana na swala hili. Katika mikataba ya kimataifa ina hatua za msingi tatu, hatua ya kwanza ni ya ku-sign pale ambapo wanachama wa umoja huo wanapokutana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya pili ni reservation na ya tatu ni lactification. Kwenye reservation ni pale ambapo nchi inaruhusiwa kutokukubaliana na baadhi ya matakwa ambayo yameelezwa lakini, katika ratification ni pale ambapo tayari mme-sign na badae mnaingia kwenye ratification kwamba mnaamua kuzi-domesticate hizo sheria ziweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanya hivyo pamoja na uchambuzi ambao umeeleza na wadau ambapo tuliwashirikisha tulibaini kwamba sisi tulikuwa mbele kidogo ya mkataba huu wa kimataifa wa mwaka 2011 kwenye masuala ya kazi, Sheria tayari sisi tunazo nchini ambazo zinaeleza utaratibu wa kazi lakini pia masuala ya mkataba na hatua nyingine maswala ya mishahara lakini pia masuala ya afya na usalama mahali pa kazi na masuala ya ifadhi ya jamii. Haya yote yapo yameelezwa kwenye mkataba lakini sisi tulikuwa tumekisha kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaenda kuangalia sasa yale ambayo yatakuwa yanautofauti na ambayo yatakuwa na tija kwa upande wetu. Kwa kweli kundi hili ni muhumu na tunaendelea kulihudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili la kuhusu mtaala wa wafanyakazi. Ni kweli Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan iliona umuhimu wa wafanyakazi wa ndani kuwa wananyanyasika sana na kwa Sheria tuliyonayo katika Kifungu cha tano cha Sheria ya Ajira na mahusuano kazini, Kifungu cha sita, cha saba lakini pia kifungu cha 11, vyote hivi vinaeleza kuhusu haki na wajibu wa wafanyakazi hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa sababu tumeanzisha hiyo program kwenye Vyuo vya VETA wewe mwenyewe utakuwa shahidi na Waheshimiwa Wabunge kwamba wafanyakazi wa ndani wananyanyasika sana kwenye maeneo mengi. Sasa tumeona kuanzisha utaratibu huo wa taaluma na kutangaza zaidi ili udahili uongezeke lakini pia kuhakikisha wanafanya kazi kimikataba na watambue na hata sisi kama wawakilishi…
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kanuni mpya ya mafao kwa wafanyakazi imekwenda kupunguza asilimia 50 ya malipo ya mkupuo ya wastaafu. Pia imepunguza miaka inayokadiriwa mtumishi kuishi baada ya kustaafu kutoka miaka kumi na tano na nusu mpaka miaka kumi na mbili na nusu.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kurejesha Kanuni ya mwaka 2017 ambayo ilikuwa imeweka maslahi mapana zaidi kwa wastaafu?

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwenye majibu ya Serikali imesema kwamba mifuko itafanya tathimini ifikapo mwezi Juni mwaka huu 2023, mpaka tunavyozungumza tayari imeshapita miezi mitano.

Je, tunaweza tukapata majibu ya tathimini hiyo ya Serikali kupitia Bunge lako Tukufu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Gambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni katika mifuko hii. Wote tunatambua tulikuwa na mifuko mingi hapo awali, mifuko ya PPF, LAPF, PSSSF na mifuko mingine mingi tu. Uendeshaji wake ulikuwa wa gharama kubwa sana kwa sababu ya menejimenti lakini ilitengenezwa katika misingi ya kuwa na ushindani. Ikawa ni wazo na mfumo wa Serikali wa kuweza kuboresha zaidi na kuangalia maslahi kwa sababu ya uhalisia na sera za wakati huo na mabadiliko ya hali ya kiuchumi ikaona ifanye actuarial evaluation ambayo ilileta majibu kwa wakati huo kwamba ilifaa kuweza kuangalia walio wengi zaidi na kuweza kuwapa manufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, asilimia 81 ya hali ya kikokotoo cha sasa inawapa manufaa ya kuwa na mkupuo mkubwa. Asilimia 19 wanabaki kuwa na mkupuo ambao ni wa wastani lakini mapato ya kila mwezi yameongezeka. Kwa hiyo, tathimini baada ya miaka mitatu ambayo tumeifikia sasa na nikijibu hoja yake ya swali la pili kwamba tunaendelea na tathimini na sasa tumpe majibu ya tathimin.

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini ni tafiti sasa huwezi ukataka kwa wakati wowote kuweza kupata majibu yake ni mpaka pale ambapo itakamilika. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ina nia njema sana kukitoa kikokotoo hiki asilimia 25 mpaka 33. Si ajabu tathimin hii itakapotoa majibu tukiangalia ustahimilivu wa mfuko na maslahi ya wafanyakazi wetu ambao ni vipenzi vya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan tutaenda kutoa faida kubwa kwa upande wao na kuweza kuwasaidia Watanzania ambao wametumikia Taifa.