Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Paschal Katambi Patrobas (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini zaidi nami nitumie fursa hii kuwapa pole Watanzania kwa msiba mkubwa uliotufika wa kumpoteza aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Zaidi ya hapo nimpe pole Mheshimiwa Rais, lakini sambamba na hilo nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini tena katika nafasi hii.

Mheshimiwa Spia, kwa sababu ya ufinyu wa muda, niende moja kwa moja na kujielekeza katika wasilisho la bajeti la Mheshimiwa Waziri Mkuu katika ofisi yake hasa kwenye maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge, lakini pia Kamati zimegusia. Nianze katika eneo moja la ajira, mchango wa ajira au nafasi zinazopatikana katika ajira.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2019 kwa maana ya kipindi cha mwaka 2015 - 2020 taarifa na maswali mengi yalikuwa yanaulizwa kuhusiana na ajira millioni nane ni kama hazipo. Sasa niwape taarifa rasmi kwamba, kwa idadi ya ajira zilizopatikana kwa awamu ya kwanza vijana kati ya umri wa miaka 15 hadi 35 ni 11,891,057 ambayo ni sawa na asilimia 52.96.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia upande wa wenye umri zaidi ya miaka 36 kwenda juu ni sawa na 10,560,488 sawa na asilimia 47.4, hii inatokana na ripoti ya taarifa ya mchanganuo wa ajira kwa shughuli na umri ya mwaka 2019 ambapo pia katika upande wa Wizara ya Fedha Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa wakati huo ambaye sasa ni Mheshimiwa Makamu wa Rais wetu, aliziandikia Wizara zote barua kuweza kutoa taarifa za kuhusiana na ajira. Hizi ndio takwimu kama zinavyojionesha hapo, kwa maana hiyo kwa kipindi hicho chote tulifanikiwa kupata ajira ya zile ambazo zilikuwa zimekusudiwa.

Mheshimiwa Spika, taarifa nyingine pia ambayo ni muhimu katika upande wetu maeneo ambayo mengi yameuliziwa zaidi ni kuhusiana na fursa ambazo vijana wetu wamekuwa wakipewa chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Katika kipindi hicho tumekuwa tukitoa mafunzo yaani internship kwa graduates zaidi ya 5,975 walikuwa wanufaika, program ya mafunzo ya ufundi stadi zaidi ya wanufaika 28,941 waliweza kupatiwa mafunzo hayo ya kujenga ujuzi na kuongeza stadi za kazi kupitia mafunzo ya uanagenzi. Pia katika program ya urasimishaji ujuzi, zaidi ya wanufaika 19,462 nao pia waliweza kunufaika na mpango huo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni mafunzo ya kilimo cha kisasa, hapa Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ilifanikiwa kupeleka vijana 136 nchi ya Israel kujifunza namna ya kuweza kufanya kilimo cha kisasa. Hao tunakwenda kuwatumia pia kama trainer, training ilikuwa kama training of trainers ambao nao pia tutawatengenezea utaratibu wa kuweza kupata ajira kwa maana ya kujiajiri na kupewa vifaa au mikopo ili waweze kujiendeleza.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika mafunzo ya greenhouse nchini kote kati ya mikoa ambayo ilinufaika, mikoa 12 zaidi ya Watanzania vijana 8,980 nao waliweza kupatiwa mafunzo hayo. Program hizi ni endelevu ikiwa sambamba na Mfuko wa Kukuza Ujuzi (skills development) zaidi ya wanufaika 1,550 wamepata mafunzo hayo.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa pili kwa kujali zaidi muda nijielekeze katika eneo hili la fursa ambazo zilipatikana za moja kwa moja. Fursa za moja kwa moja za ajira zilipatikana kwa mujibu wa taarifa iliyotoka Wizara ya Fedha, baada ya kuwasiliana na Wizara zote, ni zaidi ya 11,891,772 ikiwa ni ulinganifu wa fursa za ajira zisizo za moja kwa moja 881,354…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA): Mheshimiwa Spika, nashukuru.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwanza nikupongeze kwa sababu baada ya wewe kuchaguliwa kwa kishindo na Chama cha Mapinduzi, lakini pia kwa kuidhinishwa na Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja katika eneo la hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge. Nizungumzie kuhusu suala la Kiwanda cha Mbigiri, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba katika uwekezaji ambao unafanywa na Serikali katika mifuko hii kuna sera ambayo inaongoza uwekezaji wa Mifuko lakini pia tunayo sera ya uwekezaji ambayo ndiyo msimamizi mkuu wa Mifuko hii. Miongozo kabla ya uwekezaji ni lazima ipitishwe na Benki Kuu ya Tanzania na taratibu zinaelezwa na nini kinafanyika kabla ya uwekezaji. Mwongozo unaeleza lazima ufanyike utafiti na upembuzi ili kubaini au kugundua kama kuna economic viability yaani kuangalia faida katika uwekezaji huo.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili linaangaliwa ni katika sasa kufanya uamuzi wa kwamba uwekezaji ufanyike au usifanyike na kwa kuzingatia required rate of return ambayo inaelezwa kwenye mwongozo huo na kwa mujibu wa maelekezo mazuri yanayofanyika na Benki Kuu ya Tanzania na kigezo cha kufanya hivyo kama itaonekana kutakuwa na tija ndipo uwekezaji unaweza ukaendelea kwa kuzingatia pia miongozo ambayo inatolewa na Social Security Investment Guidelines.

Mheshimiwa Spika, sasa Social Security Investment Guidelines ndiyo zingatio la usimamizi wa Serikali katika kuhakikisha chochote kinachowekezwa kinachotoka katika Mifuko hii kiende kuleta tija. Kwa kweli niishukuru sana Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, ya Awamu ya Sita, amekuwa akitupa miongozo kwa wakati wote kuweza kuhakikisha kwamba, tunayatekeleza majukumu kama jinsi ambavyo ilikusudiwa. Nini kilitokea katika kiwanda hiki cha Mbigiri? Changamoto zilizojitokeza baada ya tafiti hizo na kuruhusiwa kuanza, kiwanda hiki ndani ya miezi 16 kilikuwa tayari kilishaanza kufanyakazi by mwaka jana mwezi Agosti kingekuwa kimekamilika.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu sote ni jambo la janga la dunia nzima, baada ya kuanza procurement procedures zilifika zikachelewa kwa sababu ya uwepo wa janga la Covid mashine zikachelewa kuingia na kufikia mwezi Agosti na sasa hivi tunavyozungumza tayari mashine zimekwisha kuingia. Kwa hiyo tunasubiri by mwezi Agosti mwaka huu pengine tayari waende kwenye hatua ya mobilization na installation kwenye eneo hilo la kiwanda.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo mkataba huu tumeendelea kuhakikisha kwamba tunasimamia ili uweze kutekelezwa kwa kadri agizo na ni siku tatu zilizopita Mheshimiwa Waziri wangu Profesa Ndalichako alikuwa kwenye kiwanda hicho na kuangalia tija namna gani Serikali itaenda kupata faida zaidi. Kwa hiyo tunalisimamia kwa karibu zaidi.

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili ilikuwa ni kuhusiana na hasara ambayo wakulima waliipata katika kilimo walichokifanya cha miwa. Sambamba na hilo tukumbuke Serikali pia nayo ililima mashamba, miwa hii yote kwa pamoja kwa maelekezo mazuri ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na uongozi wetu katika Wizara na usimamizi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu, ilibidi Serikali ifanye uamuzi wa kutafuta soko na kwenda kuuza katika viwanda vingine na miwa hii ilinunuliwa na faida ilipatikana zaidi ya bilioni moja. Kwa hiyo ilikuwa ni katika hatua ya kupunguza hasara ambayo ilijitokeza kutokana na changamoto tulizozipata.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni kuhusu madeni ya Serikali katika Mifuko. Katika hili turudi katika hoja za CAG, tulizichukua hoja 12 za Ofisi ya CAG na tayari Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri Mkuu wamekwisha kuanza utekelezaji wake na moja ya utekelezaji wa hoja hizo 12 za CAG, tayari zaidi ya shilingi trilioni mbili zimelipwa kwenye Mfuko wa PSSSF na Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan katika kupitia hiyo cash bond.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna hoja nyingine kwa kadri ya maelekezo ambayo umetupa kwamba tujielekeze katika hoja. Suala la fedha ambazo Ofisi ya Waziri Mkuu zinazosemekana bilioni 56 zinazodaiwa kwa kile alichokisema Mheshimiwa Mbunge kwamba zinadaiwa. Ni kweli fedha hizo zilichukuliwa kwa utaratibu wa kuokoa hasara ambayo kubwa walikuwa wanaenda kuipata wakulima. Ndipo Serikali ikalazimika kuchukua hatua za makusudi kuweza kuhakikisha wakulima hawa mazao yao hasa yale mahindi yananunuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, utaratibu kama jinsi ambavyo mikopo mingine inalipwa, Serikali inaendelea kulipa deni hili na Mheshimiwa Aida Khenani atakuwa shahidi hata yeye mwenyewe kuna maeneo ambayo pengine atakuwa na mkopo na mkopo unategemeana na masharti na vigezo. Kwa hiyo huwezi ukalipa kwa mkupuo, kwa hiyo hili suala tayari Serikali inalipa na niwaondoe shaka Serikali ya Awamu ya Sita katika kila hoja zinazotolewa na Wabunge na hoja zinazotolewa na Kamati za Bunge, tunazitekeleza usiku na mchana kuhakikisha kwamba maagizo ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan yanatimizwa. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia katika Bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema siku hii ya leo, na pia tangu tulipoanza shughuli hizi za Bunge. Aidha, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan ambaye kwa wakati wote ameendelea kuonesha mfano tangu alipoingia katika madaraka. Katika kipindi cha miaka miwili amefanya kazi kubwa sana ambayo Watanzania wote tunaiona na tunaishuhudia katika maeneo mbalimbali. Hata hivyo miongozo yake, maelezo yake katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa kweli sisi sote ni mashuhuda kwamba Mheshimiwa Rais amedhamiria kutuletea maendeleo katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wangu Mheshimiwa Joyce Ndalichako na Mheshimiwa Mama Mhagama ambao kwa maelekezo yao wamenisaidia sana katika kutekeleza majukumu yangu pamoja na Katibu Mkuu na Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitakushukuru wewe pamoja na Naibu Spika, Wenyeviti wa Bunge, Wenyeviti wa Kamati za Bunge na Wabunge wote kwa kutusaidia sana katika kutekeleza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, nianze kwanza kwa kusema naunga hoja mkono na vile vile kwa sababu ya muda, katika yale yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wametoa michango, maoni, mapendekezo na ushauri katika maeneo mbalimbali, niombe tu kwamba yaingie katika Kumbukumbu za Bunge (Hansard) katika taarifa yote ambayo nilipaswa kuiwasilisha.

Mheshimiwa Spika, nitaenda kugusia machache. Mengi tunayachukuwa na tunaenda kuyafanyia kazi kadri tulivyoelekezwa na kushauriwa na Waheshimiwa Wabunge. Lipo suala la fedha za ukarabati wa Vyuo vya Watu Wenye Ulemavu na Utangamao. Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya jukumu hilo na ilitekeleza na tumeendelea kutekeleza na mpaka sasa tunavyozungumza, kwa mafanikio makubwa Mheshimiwa Rais ametusadia kuweza kufufua vyuo zaidi ya saba ambavyo vilikuwa viko hoi, kwa zaidi ya miaka 10 vilikuwa havifanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, tayari Chuo cha Masiwani Tanga kimefunguliwa, kinafanya kazi na wanafunzi ambao ni Wwatu Wenye Ulemavu tayari wameshaanza kupata mafunzo. Chuo cha Luanzari pale Tabora tayari kimeshaanza kufanya kazi, pia Chuo cha Saba Saba Singida, Mtapika Mtwara, na Chuo cha Yombo. Vyote hivi ni kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais amefanya kwa ajili ya Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Spika, vile vile, katika maeneo hayo, pia katika hoja nyingi ambazo za Waheshimiwa Wabunge zilizoelekeza kwamba tuangalie katika kutoa unafuu kwa watu wenye ulemavu, nawashukuru sana kwa michango yao, lakini pia Mheshimiwa Rais alitoa fedha zaidi ya Shilingi milioni 60 ambazo zimeendelea kutolewa kwenye mwaka wa fedha kuwasaidia watu wenye ulemavu kupata mafuta yale maalum ya ngozi. Vile vile kana kwamba haitoshi Mheshimiwa Rais kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na kwa maagizo ya Mheshimiwa Rais na maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, tayari tumeshashaandaa mwongozo maalum ambao unawataka kutoa 3% kwa watu wenye ulemavu ya ajira zote ambazo zinatangazwa. Kama mmeona Mheshimiwa Rais ameendelea kutoa ajira na watu wenye ulemavu tumeendelea kuwapa kipaumbele katika kutoa ajira kwa kufuta mwongozo huo unaotutaka katika ajira zote zinazotangazwa 3% angalau iwe ya watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, pia katika upande ya watu wenye ulemavu, kwenye eneo lingine, tumeweza pia kufanikiwa kupitia Mheshimiwa Rais, ameweza kuchukua Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu (SHIVIAWATA) na yeye mwenyewe aliwaalika Ikulu ya Chamwino na zaidi ya hapo akatoa ahadi ya kutoa kiwanja kwa ajili ya kujenga Makao Makuu ya Watu Wenye Ulemavu hapa Dodoma. Mheshimiwa Rais ameshaanza kutekeleza, ametoa kiwanja chenye thamani ya Shilingi milioni 37 kwa ajili wa utekelezaji wa shughuli za watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia lilikuwepo suala lingine la kuhusiana Serikali iweke mikakati ya kukusanya maduhuli kufikia lengo ambalo lilikusudiwa. Katika ukusanyaji wa maduhuli, Ofisi ya Waziri Mkuu tunaipata kupitia vibali vya kazi. Hapa tayari mpango umeshafanywa na tumeshaanza mkakati wa kuangalia namna gani tutaongeza ufanisi katika utekelezaji wa jukumu hilo.

Mheshimiwa Spika, tunatarajia kupata magari 17 ambayo yatafanya kazi ya kufanya ukaguzi kwenye maeneo ya kazi ili kuhakikisha kuna kazi za staha, lakini pia kuna afya na usalama mahali pa kazi na hivyo tutaweza kukusanya tozo na ushuru. Sambamba na hilo, katika sheria yetu inayoratibu ajira za wageni ambayo inataka ada zinazotolewa na watu wanaoomba ajira hawa, wamekuwa wakilipa ada na kwa sababu ya uratibu huu, na kwa sababu ya kufungua makampuni na uwekezaji mkubwa kwa Taifa letu, kumepeleka sasa kuweza kusaidia zaidi kwamba tunaweza tukafikia malengo yaliyokusudiwa kwenye kukusanya maduhuli ambayo tunayakusudia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mikakati ambayo imewekwa pia ni pamoja na kuongeza kupitia Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora ni pamoja na kuongezea uwezo OSHA kwa maana ya kutoa ajira. Kibali cha ajira kimetoka kwa wafanyakazi zaidi ya 18 ambao tunatarajia wataajiriwa na kuweza kuongeza fedha katika uratibu wa shughuli za OSHA katika maeneo kuhakikisha kwamba lile jukumu la Ofisi ya Waziri Mkuu la kuhakikisha kuna kazi za staha nchini linatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine kama nilivyoeleza ambazo tutazijibu tu; moja ni hii ya kwamba Serikali iongeze bajeti katika program ya kukuza ujuzi. Lengo la Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2015 kwenda 2025 tunakusudia kutoa mafunzo kwa Watanzania zaidi ya 681, na katika kufanya hivyo itakuwa ni kwa kipindi cha miaka mitano. Tayari Wizara ya Fedha imeji-commit kwamba tutaendelea kupata fedha kwa ajili ya kuhakikisha mafunzo haya yanafanyika. Pia kumekuwa na program mbalimbali za ukuzaji ujuzi ambapo kwa mwaka wa fedha 2021/2022 tulipata zaidi ya Shilingi bilioni tisa ambazo zilienda kuwasaidia vijana wengi wa Kitanzania kuweza kupata mafunzo kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, pia lilikuwepo suala lingine la kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kutoa program hizi za mafunzo. Wapo wadau wa maendeleo ambao tunashirikiana nao; GIZ, International Labour Organization na IOM ili kuona kam tunaweza kushirikiana katika masuala ya kibajeti ili kuweza kuendelea kuboresha na kuhakikisha kwamba tunapata fursa, na pia kuwapa fursa Watanzania wengi katika kupata mafunzo mbalimbali yanayohusiana na kukuza ujuzi na pia kuwaandaa katika kukabiliana na soko la ajira.

Mheshimiwa Spika, pia lipo suala lingine la fursa za ajira nje ya nchi. Hili tumeshaanza kulifanya. Kama tulivyoeleza pia kwenye hoja za Kamati na Waheshimiwa Wabunge kupitia Wakala wa Ajira Nchini (TAESA) ambapo tayari tumeshasajili na kupitia kamishna wa kazi. Tumeshasajili Wakala wa Ajira ambao wanatafuta ajira ndani na nje ya nchi na kwa kufanya hivyo, tayari tumeingia bilateral agreement na nchi zaidi ya nane ambayo tunaingia nao katika majadiliano ili kuweza kuona namna gani tunaweza kupata fursa zaidi za kuwasaidia Watanzania wengi kuajiriwa nje ya nchi na kutengeneza utaratibu maalum wa kuwasajili wale walio nje ya nchi waliopata ajira ili tuweze remittance ambayo ni sehemu ya mapato pia katika Serikali.

Mheshimiwa Spika, pia kwa kumalizia, lipo suala ambalo Waheshimiwa Wabunge walilizungumzia kuhusiana na kuweka kumbukumbu za hawa watu walioajiriwa nje ya nchi. Tayari tumeshaandaa mfumo maalum wa kieletroniki wa wao kuweza kujisajili na pia tunawasajili wale ambao wanatafutiwa na wakala mbalimbali wa ajira ili kuweza kuwa na kanzidata ambayo itatusaidia katika kuwaratibu na pia kusimamia haki zao huko wanapofanya kazi nje ya nchi. Vile vile kazi zote ambazo ni za nje ya nchi tunataka tuziratibu vizuri ili kuepusha Watanzania wengi kwenda kudhalilishwa ama kuumizwa ama kutendewa matendo yasiyofaa wakiwa nje ya nchi. Hilo ni jukumu ambalo tumeshaanza kulifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuhusiana na maendeleo ya vijana; hapa katika kuboresha kulingana na michango ya Waheshimiwa Wabunge na Kamati, tayari tumeshadilisha miongozo. Mwongozo wa utoaji wa mikopo ule wa asilimia 10 katika Halmashauri, sasa kijana mmoja anaweza kupata mkopo na ni kuanzia Shilingi milioni 10 mpaka milioni 50. Vile vile kwa watu wenye ulemavu, mikopo hii nayo pia inatolewa kwa mapato ghafi ya Halmashauri na tayari mabadiliko ambayo tumeshayafanya huko, ni kuhakikisha pia watu wenye ulemavu kulingana na changamoto zao, ilikuwa ngumu kufanya kazi wakiwa watano, lakini sasa tumefanya mabadiliko, hata mtu mmoja pia anaweza kupewa mkopo kwenye ngazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye eneo hilo, Mfuko wa Maendeleo ya Vijana tunazidi kuuboresha sasa tuweze kuona ni namna gani tutawafikia vijana wengi zaidi kuweza kuwasaidia: Kwanza, kuwapa mafunzo kama yale ambayo wanamaliza walio wahitimu wa vyuo vikuu, kuwatambua waliko, kutambua kada mbalimbali ambazo wamezisomea, kuwasajili TAESA na kuwapeleka kwa waajiri ili wakapate mafunzo ya utayari wa kufanya kazi kwa maana ya internship. Tayari tumeshapeleka vijana zaidi ya 6,000 kwenye maeneo mbalimbali na wanachangiwa fedha kidogo na Serikali zaidi ya Shilingi 150,000 kwa mwezi kwa ajili ya kuwaandaa.

Mheshimiwa Spika, lakini vile vile nikimalizia kwa sababu ya muda, mambo ni mengi na kwa sababu hoja hizi tayari ziko hapa ziweze kuingia kwenye Hansard, Mheshimiwa Rais ameendelea kuweka mpango wa kuwaangalia vijana katika maeneo mbalimbali. Fedha za Bodi ya Mikopo, hizo nazo ni fedha ambayo ni sehemu ya kuwasaidia vijana, kuwaratibu. Zaidi ya Shilingi bilioni 570 ziliongezwa, pia fedha za Halmashauri, zote hizi zinawasaidia hao vijana ambao tumekusudia kuwasaidia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya, ahsante sana.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, pamoja na kupeleka mafunzo ya utaifa, uzalendo lakini pia maadili na kuweza kusaidia Taifa kuweza kuwaandaa vijana ambao ni nguvu kazi ya Taifa ya hivi sasa na hata ya baadaye.

Mheshimiwa Spika, ahsante, mengine Waheshimiwa Mawaziri watanisaidia katika kuweza kuyajumuisha.

MHeshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nami niungane na wenzangu katika kuwapongeza sana Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kufanya kazi nzuri sana, sana, sana ambazo zimekuwa reflected kwenye takwimu na taarifa mbali mbali. Vile vile nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa hali na azma yake kubwa ya kutamani kuona Tanzania ikikua kiuchumi kwa kubadilisha sheria mbalimbali na pia kubadilisha mifumo na kutengeneza mazingira mazuri kwa ajili ya uwekezaji ndani ya nchi yetu. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nampongeza pia hasa kwa kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara miradi ambayo imesajiliwa kwa kipindi hiki tu kifupi; ukiangalia mwezi Julai, 2022 mpaka Machi, ni zaidi ya miradi 240, ambayo thamani yake ni Dola za Kimarekani milioni 438 na hii imesaidia sana katika kukuza uchumi. Sambamba na hilo, kumekuwa na ongezeko la ajira watu zaidi ya 39,245 ambao wamenufaika na ajira katika usajili wa miradi hiyo mipya.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Rais pia ameweka mikakati mbalimbali ya kukuza ajira. Moja ya mikakati ni hili la kuweza kukuza viwanda hasa katika suala la kwenye sekta ya uwekezaji. Tumebadilisha sheria, na pia tumerahisisha mazingira ya uwekezaji nchini kuweza kuwa rahisi zaidi ili uwekezaji ukue na kuweza kupata kipato. Nchi nyingi duniani leo zimetoka kwenye masuala ya kufanya biashara kwa maana ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, Serikali sasa imekuwa inatengeneza mazingira wezeshi na kukusanya kodi. Vile vile sehemu kubwa ya biashara, mfano ajira zinatokana zaidi na private sector ambayo sasa hivi Mheshimiwa Rais ameamua kui-enhance kwa sehemu kubwa sana, tunaona kwenye kilimo mapinduzi makubwa; kwenye uwekezaji tunaona mapinduzi makubwa; na kwenye viwanda tunaona uwekezaji mkubwa ambao unafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika upande wa ajira, tunaweza kuona kwa upande wa ajira za kisekta ni maagizo ya Mheshimiwa Rais na maelekezo mahususi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba Wizara zote za kisekta lazima kwenye mwaka wa fedha unazopewa bajeti, zizalishe ajira ili Watanzania waweze kunufaika na ajira hizo katika ngazi mbalimbali. Hilo limekuwa likitekelezwa.

Mheshimiwa Spika, vile vile katika miradi tu ya Wizara za maendeleo, zaidi ya Watanzania 1,226,925 walipata ajira. Sasa kwa muktadha huo huo wa spirit ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuongeza ajira, kukuza uchumi na kutengeneza uchumi jumuishi ili kila mwananchi aweze kunufaika, ni pamoja na kutengeneza mazingira ya kuwasaidia wawekezaji, na pia kusaidia kwenye sekta ya uchumi ya biashara ili iweze kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, nimesikia hili suala la Tanga ambalo limesemwa sana na Waheshimiwa Wabunge hapa. Nimelazima kufuatilia kwa sababu limegusa hasa kwenye sekta na Wizara yetu ya kwenye masuala ya ajira. Ni kweli nimefanya utafiti na nimeangalia kwenye rekodi mbalimbali zilizofanywa ikiwa ni pamoja na hesabu za kihasabu zilizofanywa kwenye Kampuni ya Tanga Cement, inathibisha kwamba Tanga Cement haina uwezo tena wa kujiendesha, ina-run kwa hasara. Zaidi ya hapo, hata fedha zile ambazo inazipata kidogo katika operation, inajikuta inashindwa kulipa kodi; na kwenye eneo la kodi lazima uangalie kama ni faida. Unaangalia faida ghafi ambayo ni jumla ya gross profit, na pia utaangalia net profit baada ya operational cost. Pia utaangalia gharama nyingine ambazo utazipata kama unapata faida baada ya kulipa kodi, na vile vile utaangalia kabla ya kulipa kodi na baada ya kulipa kodi. Hizi zote zinathibitisha kampuni hiyo haina uwezo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, katika maamuzi ambayo yalifanyika, FCC katika malalamiko yaliyopelekwa tarehe 2 Novemba, 2021 FCC iliamua kwa misingi miwili ambayo imeainishwa kwenye Sheria Ushindani ambapo katika Kifungu chake cha 5 (6) (a) na (b) kinatoa masharti kwamba kampuni haipaswi kuwa na nguvu kubwa kwenye soko, lakini pia (yenyewe peke yake) isiwe na uwezo ambao unaweza kuathiri watu wengine kufanya biashara. Katika tafsiri ambazo zilitumika FCC, waliweza kuzingatia matakwa pia ya Sera ya Taifa na pia mwendendo na mtazamo wa Serikali ya Awamu ya Sita, na pia katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi inayotaka kukuza uchumi wa Taifa, uchumi wa Watanzania na mtu mmoja mmoja na pia kukuza uchumi jumuishi na kutengeneza fursa za ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kipengele kilichotumika waliangalia muktadha huo na kuona kwamba katika kipengele cha 5 (a) kinachohitaji nguvu ya soko, ambayo kwa lugha ya kigeni inasema ni sales volume ambayo inahitaji isizidi asilimia 35, ndicho kigezo pekee ambacho kilionekana. Sheria hii katika kipengele cha pili inahitaji pia huyo mtu ili aweze kuonekana ana dominance kwenye soko, ni lazima awe amekidhi vigezo vyote katika kifungu cha 5 hicho, kipengele (a) na (b).

Mheshimiwa Spika, tafsiri iliyofanyika katika Fair Competitions Tribunal, wao walijikita zaidi kwenye kigezo kimoja tu cha installed capacity ambapo waliangalia katika kipengele cha asilimia 35 bila kuangalia kwamba sheria inataka vyote kwa pamoja vitamkwe kama jinsi sheria inavyosema katika kifungu hicho. Kwa hiyo, wakafanya maamuzi ya ku-crash decision ile na kusema kwamba maamuzi ya FCC yaondolewe na muunganiko huo usiwepo.

Mheshimiwa Spika, sheria hiyo hiyo pia katika kifungu chake cha pili inaitaka mamlaka katika kutafsiri sheria; haitafsiri katika mazingira yale, na ni principle ambayo hata kwenye sheria ipo, ya kusema kwamba every case should be judged from its own circumstances, kwamba kila kesi lazima iangaliwe na kutafsiriwa kwa mazingira yake kama jinsi ilivyo. Katika msingi huo huo, hata kwenye Sheria za Kiuchumi pia maamuzi yanaangaliwa kutokana na jinsi ambavyo hali ya kiuchumi, na mazingira yaliyokuwepo kwa wakati huo.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka 2020, maamuzi yaliyofanywa na FTC (Fair Competition Tribunal), wao walifanya uamuzi kwa ku-base zaidi na tafiti ambazo zilifanyika katika kipindi cha mwaka 2020. Hali ya sasa hata ukiiangalia, mwaka 2020 aliyekuwa anaongoza kama kiwanda kwenye kupata mengi na uzalishaji ilikuwa ni Twiga Cement anafuatiwa na Tanga Cement na Dangote. Kwa hali ya 2022 kwa tafiti zilizokuja kufanyika na takwimu kwa mujibu wa data ambazo zipo, inasema anayengoza kwa sasa, siyo kama ilivyokuwa 2020 tena, takwimu zinaonesha sasa Twiga Cement ndiyo anaongoza, anafuata Dangote na kuna kiwanda kingine ambacho hakikikuwepo kabisa kwenye soko, wakati huo kilikuwa hakizalishi, kilikuwa kinaanza, lakini sasa kinazalisha zaidi ya tani 900,000, ambacho ni Kiwanda cha Shuwan Maweni na kiwanda kingine ambacho kinafuata sasa ndiyo Tanga ambacho bado pia kinashuka katika uzalishaji, ambacho ndiyo maana ya maombi haya kuweza kufanya uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, mwekezaji huyu amekuwa anazalisha na anafanya kazi ya kuzalisha cement za Twiga lakini pia anaenda kuingiza capital, ku-inject new capital ya zaidi ya Shilingi trilioni moja ili kuongeza capacity. Katika maamuzi yaliyotolewa awali ya FCC, yalikuwa na masharti. Masharti hayo yalikuwa kumi, kati ya masharti matatu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba dakika moja nimalizie.

SPIKA: Utakuwa unachukua muda wa Waziri hapo. Malizia dakika moja.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, katika masharti hayo yaliweza kukubaliwa pia na hao wadau wa maendeleo. Zaidi nimalizie tu kwa kusema kwamba, hili jambo siyo jipya. Ipo kesi ya Afrika Kusini ya mwaka 2019 na imefanyiwa maamuzi, ambapo kesi hiyo ilikuwa hivyo hivyo kwamba walirudi tena katika kufanya review baada ya maamuzi ya awali. Kwa hiyo, hakuna suala la kudharau Mahakama au maamuzi hapa. Suala lipo, linatoa haki. Sheria hiyo ni kwamba unaweza ukarudi tena kupeleka maombi kulingana na hali iliyopo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, kuna kesi nyingine pia ya Toyota na Sifao Motors, ambayo nayo pia ilifanyiwa maamuzi hivyo hivyo na FCC ikakataa ombi lao, lakini pia ilivyokuja kurudi FCT, nayo pia ilikuja ikabariki maamuzi yaliyofanywa na FCC. Kwa hiyo, jambo hili siyo geni, tunachelewesha uwekezaji, tunachelewesha Watanzania kuweza kupata uchumi, tutaenda kupata hasara ya kupoteza ajira 3,000 za Watanzania, tutaenda kupata hasara za uwekezaji wa kukosa zaidi ya Shilingi trilioni moja kama maamuzi haya tutaenda kuyafanya kishabiki na bila kuangalia maslahi ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono kwamba suala hili la uwekezaji ni muhimu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema, pia nishukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniteua na kuniamini na kunipa dhamana ya kuweza kuwatumikia Watanzania, ninamuahidi yeye pamoja na viongozi wengine Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba nitatekeleza majukumu yangu kwa uaminifu, uadilifu lakini katika kusaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nikupongeze na kukushukuru pia wewe kwa kuendesha Bunge lako vizuri pamoja na uongozi wote wa Bunge aidha niwapongeze pia Watumishi wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu ambao wametusaidia katika majukumu mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, ninaupongeza muhimili wa Mahakama na viongozi wengine pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuendelea kulisimamia Taifa letu kuwa salama.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda nijielekeze katika mambo ambayo yamezungumzwa zaidi au yamechangiwa zaidi na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, nikianza na eneo la ajira. Ofisi ya Waziri Mkuu mbali na majukumu mengi yaliyopo inalo jukumu pia la kuweza kuhakikisha kwamba inasimamia na kuratibu Sera pamoja na sheria zote zinazohusika na masuala ya ajira. Katika msingi huo tunamshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa akituelekeza wakati wote tuweze kuwapokea, kuwasikiliza pia kuwahudumia wale wote ambao wanafika katika ofisi hiyo kwa ajili ya kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, katika study ambazo tumejaribu kuzifanya ili kutafuta ulinganifu na suluhu ya changamoto za masuala ya ajira nchini, Ofisi ya Waziri Mkuu na kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Waziri wangu wa nchi Professor Joyce Ndalichako pamoja na watumishi tumejaribu kufanya study na ulinganifu mbalimbali katika kuangalia changamoto za ajira kwa nchi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tumeweza kufanya utafiti wa kuangalia na kuandaa taarifa ya uchambuzi wa sera, sheria na mikakati ya nchi mbalimbali kuhusu utatuzi wa changamoto za ukosefu wa ajira. Katika maeneo ambayo tumejaribu kuangazia mojawapo ilikuwa ni nchi ya Uganda, Rwanda, Brazil, China Marekani, Tunisia, Uturuki, South Afrika na Kenya.

Mheshimiwa Spika, katika maeneo hayo yote ambayo tumefanyia utafiti wenzetu wamefanana pia maeneo mengi na sisi lakini sisi pia tumeenda hatua ya mbali zaidi. Changamoto kubwa ambazo zinaonekana katika wimbi hili kubwa la ukosefu wa ajira, ambalo sehemu nyingi wanaita kama timing bomb duniani, sababu zinazosababisha ukosefu au changamoto ya ajira nyingine ni chanya na nyingine hasi.

Mheshimiwa Spika, sababu ya kwanza ni ongezeko la taasisi za elimu kwa maana ya uhamasa katika kusoma, kumekuwa na wahitimu wengi katika kada mbalimbali tofauti na uhitaji wa ajira. Sababu ya pili ya kidunia inayoelezwa katika takwimu mbalimbali za International Labour Organization kwa maana ya shirika la kazi duniani, pamoja na taasisi nyingine ni uwepo wa advancement ya teknolojia.

Mheshimiwa Spika, uwepo wa teknolojia umeenda ku-replace human labor, kwa maana ya computer au mashine sasa inaweza ikafanya kazi ya watu zaidi hata ya
100. Sababu nyingine imeelezwa ni masuala ya natural catastrophic na force majeure - acts of God pamoja na masuala kama ya magonjwa kama vile COVID-19 ambayo imesababisha viwanda vingi kufungwa na changamoto nyingine pia makampuni na kadhalika kuweza kufilisika.

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ni masuala ya sasa biashara kiujumla duniani, Serikali zimeacha kufanya shughuli ya biashara na badala yake zinatoa huduma, kwa hiyo biashara imelekezwa katika private sector. Jingine ambalo limeelezwa katika takwimu ni masuala ya viwango vya elimu inayotolewa, mtu apate skill na knowledge competence and performance ya kuweza kufanya kazi. Kwa hiyo, wanapimwa kulingana na ubora na hizo ndio wakati mwingine vimekuwa ni vigezo vya kuweza kusaili watu.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kimefanyika kwenye Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika eneo hili na katika kutafuta njia mbadala sasa za kukabiliana na changamoto hizo. Kwanza katika kufanya hivyo tulifanya pia utafiti wa kuangalia wingi wa vijana wengi ambao wanaingia katika soko la ajira kila mwaka. Katika tafiti tulizozifanya ukiangalia kwa darasa la saba ukiacha kwa sababu ya muda nisianze mwaka 2012 mpaka mwaka 2021 niende kwenye mwaka 2021 peke yake.

Mheshimiwa Spika, wahitimu wa darasa la saba walikuwa milioni moja na laki moja, kidato cha Nne ni Zaidi ya laki nne na themanini na saba elfu, kidato cha sita ni zaidi ya wahitimu elfu themanini, walioweza kufuzu mafunzo ya VETA ni zaidi ya laki mbili na thelathini na sita na FDC Wahitimu Zaidi ya elfu kumi na moja, lakini pia NACTE ni wahitimu elfu themanini na saba. Kwa ujumla ukienda kwenye vyuo vikuu peke yake kwenye soko wanaingia 47 elfu katika soko la ajira.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kwa sababu ukija kuangalia katika ujumla wake tuna watu zaidi ya laki moja wanohitaji ajira katika soko tofauti na hitaji lilivyo.

Mheshimiwa Spika, hatua tulizozichukuwa Ofisi ya Waziri Mkuu ni:

Moja; kuandaa na kutengeneza uwepo wa vyuo vya VETA kama jinsi China walivyofanya vyuo vikuu zaidi ya laki sita wamevibadilisha na kuwa vyuo vya kati kuweza kutoa mafunzo na skills za kazi.

Pili; tumeendelea kutoa fedha za mikopo za kuweza kuwasaidia katika ngazi za Halmashauri na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ili waweze kupata mitaji ya kuweza kufanya shughuli mbalimbali.

Tatu; kumekuwa na mkakati wa kutengeneza mfumo wa ukuzaji wa ujuzi wa vijana ambao wamekuwa wakitoka vyuo vikuu na wale ambao hawajarasilimishiwa ujuzi, tumekuwa tukitoa fedha kwa ajili ya kurasimisha ujuzi na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa mwaka wa jana alitoa zaidi ya bilioni tisa ilinufaisha vijana zaidi ya 14,440 katika mafunzo.

Mheshimiwa Spika, pia kuna mafunzo ya...

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika,
ahsante sana kwa nafasi hii. Ninashukuru sana nami niungane na wenzangu kuwapongeza sana Wizara ya Ulinzi lakini pia nimshukuru na kumpongeza sana Amiri Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuiongoza Nchi yetu vizuri na mpaka sasa tunaona amani na salama tunayo na tunaendelea kujenga uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru pia wewe kwa kunipa nafasi hii zaidi nichangie tu kidogo kwenye eneo moja, Kwanza niwape confidence ya Serikali kwenye eneo hili, imezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge vizuri sana hapa kuhusiana na hoja mbalimbali wote ni nia njema ya kutaka kuboresha vyombo vyetu hivi vya ulinzi na usalama na hasa Jeshi letu hili.

Mheshimiwa Spika, Vyombo vya Ulinzi na Usalama vinatambulika kwenye Katiba kwa mujibu wa Ibara ya 147 (1) na (2) lakini pia ni jambo ambalo liko kwenye orodha ya Muungano katika orodha namba tatu na sambamba na hilo vyombo hivi vya ulinzi na usalama Amiri wake Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 148 ya Katiba ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na si mwingine ni Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatambua Serikali upande wa umuhimu kubwa wa Jeshi hili la kwetu hapa la ulinzi na usalama, kwa kutambua umuhimu huo kwa sababu jeshi hili limefanya kazi kubwa ya kulinda mipaka ndani na nje ya nchi lakini pia kulinda viongozi wetu, kulinda uchumi wetu ili isitokee wakati wowote hali ambayo itapelekea kupoteza usalama wa Nchi na hivyo kurudi nyuma katika uchumi na hata kupoteza maisha au usalama wa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala hilo niweze kueleza tu kwenye maeneo ambayo yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge. Kwanza limezungumzwa hapa suala la kuhusiana na kodi. Niwape tu uhakika na kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba michango yote ambayo wameizungumza hasa kwenye maeneo ya kodi kwenye vifaa vya Jeshi lakini pia maslahi megine ya vyombo vyetu hivi vya ulinzi na usalama si yote ambayo tunaweza tukayazungumza hadharani hapa, kwa sababu Bunge lako Tukufu hili linaenda public, lakini kuna mambo niwahakikishie na kuwapa confidence Waheshimiwa Wabunge kwamba kama Serikali tumeyachukua tunaheshimu sana na kupokea mchango wao kwa moyo mkunjufu ili tuweze kufikisha na viongozi hawa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana husika atakutana na Waziri wa Fedha lakini pia wataongozwa na viongozi na timu nzima, kwa ajili ya kuyaangalia pia masuala haya ya kikodi yamekaaje na kuweza kuyaweka sawa sawa ili kuimarisha Jeshi letu ambalo lina heshima kubwa sana ndani na nje ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, mnakumbuka kwenye peace keeping mission mara nyingi Tanzania tumekuwa tukipata record nzuri sana ya kufanya vizuri katika kazi za Kimataifa ambazo zimekuwa zikitokea katika Ukanda wa Afrika hata katika ngazi ya Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunatambua kwenye eneo lingine la masuala ya wastaafu ambao ni Wanajeshi, wanapopumzika sasa tunatambua wanakuwa wamechangia na wamefanya kazi kwa kweli kubwa kwa kuweka mchango wao kwa masuala ya kiusalama lakini pia ujenzi wa Taifa katika suala la uchumi. Mimi pia katika eneo hili nieleze na kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwa sababu Mawaziri wenye dhamana husika hapa pengine hawapo lakini kwa hatua hii kwa sababu sisi tuko hapa kuwakilisha hili, tunalichukua nalo na tutaenda kufanya kazi ya kufanya mapitio upya ya wastaafu wetu wa vyombo vya ulinzi na usalama ambao bado wana changamoto za kuhusiana na kupata mafao yao au kupewa stahiki zao ili kuweza kuhakikisha kwamba basi tunaona na kuheshimu mchango wao katika kipindi chote ambacho wamefanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia katika maeneo mengine ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na suala la fursa za ajira kwa ajili ya vijana wetu na namna ya kuweza kuunganisha na kutengeneza teamwork pamoja na Jeshi hili kwa maana ya Wizara ya Ulinzi. Hili nalo tunalichukua kwa ajili ya kulifanyia kazi na hivi yote ni kwa sababu ya maslahi mapana ya Taifa letu lakini nizidi kuhakikishia Watanzania wote wanaonisikiliza lakini pia Bunge lako Tukufu. Sisi Serikali tuko imara tukiongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye Amiri Jeshi Mkuu katika vyombo vya ulinzi na usalama wakati wote, tutasikiliza kwa unyenyekevu na tutaenda kutoa huduma inayostahiki kwa mujibu wa mambo yale ambayo yatakuwa yamepangwa ili kuweza kuhakikisha mipango na mikakati inawekwa sawa sawa ili kuweza kuhakikisha Taifa letu linakuwa salama pia tunaendelea kuulinda uchumi wetu wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatutakuwa na uchumi wala hatutakuwa na shughuli kama usalama utakuwa hatarini, kwa hiyo usalama ni kipaumbele namba moja cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa muda wako, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)