Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Neema Kichiki Lugangira (34 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyo mezani ya hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. Napenda kujielekeza katika sekta ya kilimo na hivyo nitaendelea kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake na naomba nifanye rejea kwenye ukurasa wa 25 alisema kwamba: “kwenye miaka mitano iliyopita tumefuta tozo 168 ambapo 114 zilihusu kilimo, mifugo na uvuvi na 54 za biashara. Tutaendelea na hatua hizo.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kufanikisha hili ambapo lengo kuu naamini ni kuimarisha uwekezaji na hivyo hivyo punguzo hizi zinaweza kuimarisha na kunufaisha wakulima wadogo. Hivyo napenda kuishauri Serikali kuwa ni muhimu sasa kufanya tathmini ili tuweze kujiridhisha punguzo za tozo hizi zote kama zinanufaisha wakulima wadogo kama ambavyo tunatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niiombe Serikali iagize wadau wote kufanya impact assessment ya tozo zote ambazo tumetoa, maana kwa uzoefu wangu inaonekana kwamba saa nyingine tozo hizi kunakuwa hakuna trickle- down effect ya kufika kwa wakulima wadogo ipasavyo. Mimi naamini kwamba uimarishaji wa mazingira ya ufanyaji biashara unatakiwa uende sambamba na unufaikaji wa wananchi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake kwenye ukurasa 26 naomba kunukuu, alisema: “Kwa msingi huo kwenye kilimo mathalani tunakusudia kuongeza tija na kufanya kilimo chetu kuwa cha kibiashara. Lengo ni kujihakikishia usalama wa chakula, upatikanaji wa malighafi za viwandani na pia kupata ziada ya kuuza nje. Ili kufanikisha hayo, tutahakikisha pembejeo na zana bora za kilimo ikiwemo mbegu, mbolea, viuatilifu/ dawa na matrekta vinapatikana kwa uhakika na gharama nafuu.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, kwa mara nyingine tena napenda kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa iliyofanya kwa miaka mitano iliyopita. Hotuba ya Mheshimiwa Rais imesisitiza yale ambayo yameandikwa kwenye Ilani ya chama tawala, Chama cha Mapinduzi kwenye kifungu 35 – 46. Hivyo ili tuweze kufanikisha haya kwa kasi ambayo inatakiwa ningependa kushauri yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, ni lazima sasa tujikite katika uzalishaji wa aina mbalimbali za mbegu maana hivi sasa ukienda kwenye duka la mbegu utakuta 80% ya mbegu hizo zimetoka nje ya nchi na hivyo Tanzania tunakosa soko kubwa la uzalishaji wa mbegu. Aidha, naishauri Serikali iweke kipaumbele cha kujengea uwezo taasisi zetu za ndani na za binafsi za ithibati (Local Certification Boardies). Kwa kufanya hivi, tutaweza kufanikisha mbegu ambazo tunazizalisha ndani ya Tanzania nazo ziweze pia kuuzwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, vivyo hivyo jambo langu la tatu, nakubaliana na mapendekezo yaliyo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuhusu Wizara ya Kilimo kuwa na bodi za mazao na taasisi ambazo zinahitaji kupitiwa upya kimuundo ili ikiwezekana kuwe na taasisi chache zitakazoongeza ufanisi na kuimarisha usimamizi wa sekta hii. Nimesema hivi kwa sababu kwa jinsi ilivyo sasa wingi wa hizi bodi za mazao na taasisi unaleta mkanganyiko mkubwa kwenye sekta hivyo unakinzana na dhana nzima ya kuimarisha mazingira wezeshi ya uwekezaji na biashara kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, mwisho niapenda kutoa wito kwa wadau wa sekta ya kilimo kuwa mstari wa mbele kuhamasisha uzalishaji na ulaji wa vyakula vyenye viini lishe vingi ili kuungana na jitihada za Serikali za kutokomeza udumavu na utapiamlo kwa ujumla. Kama ambavyo tunafahamu Waheshimiwa Wabunge Tanzania 32% ya watoto chini ya umri wa miaka mitano wamedumaa, kwa maana hiyo katika kila watoto 100 watoto 32 wamedumaa. Cha kushangaza zaidi mikoa inayoongoza kwa udumavu ni mikoa ambavyo inaongoza kwa uzalishaji wa chakula (food basket). Ndiyo maana nimesema tutoe wito kwa wadau hawa pamoja na kuhamasisha uzalishaji wa mazao ya kibiashara pia wahamasishe uzalishaji na ulaji wa mazao yenye viini lishe vingi ambayo imo kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru tena kwa fursa hii ya kuchangia hoja iliyo mezani na naunga mkono hoja ya hotuba ya Mheshimiwa Rais, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo kwa mara zote amekuwa akiibeba agenda la local content na akiendelea kusisitiza umuhimu wa kuongeza na kuimarisha ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hizi za uziduaji ikiwemo na sekta ya madini.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu nitajielekeza kwenye ule mradi wa Kabanga Nickel uliopo Wilayani Ngara Mkoani Kagera, hapa napenda nitambue jitihada kubwa sana za Mhashamu Baba Askofu Niwemugizi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Ngara Kaka yangu Mheshimiwa Ndaisaba wamejitahidi sana kulisemea suala hili kwamba kwenye mradi huu wa Kabanga Nickel yanachimbwa yale madini lakini yatasafirishwa na kufanyiwa uchenjuaji Kahama, jambo ambalo tukirudi kwenye misingi ya local content itafifisha namna ambavyo wananchi wa Ngara na Mkoa mzima wa Kagera kwa ujumla watakavyonufaika na mradi huu wa Kabanga Nickel. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa lugha nyingine ni kwamba Mkoa wa Kagera na Wilaya ya Ngara yatabaki mashimo wakati fursa zote ambazo ndiyo nyingi za wananchi wa Ngara na wananchi wa Kagera kwa ujumla kuweza kushiriki zitahamishiwa Wilayani Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo ningependa kupata maelezo ya kina kutoka kwa Serikali kwanini wameamua kwenda kinyume na ambavyo inatakiwa kwamba katika mnyororo wa mradi, mnyororo mzima wa mradi unatakiwa ufanyike katika eneo la mradi. Kwanini katika mradi huu wa Kabanga Nickel Serikali imeamua kuchimba Wilayani Ngara ambako mradi ndiyo upo na madini ndiko yalipo lakini kuwekeza refinery Wilaya ya Kahama Mkoa wa Shinyanga.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hilo litafifisha ushiriki wa wananchi wa Ngara, litafifisha ushiriki wa wananchi wa Kagera, litafifisha fursa za wanawake, vijana na jamii nzima ya Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili wote tunafahamu kwamba kuna kitu kinachoitwa service levy asilimia 0.3, hii service levy itakuwa inakwenda Kahama, sasa Je, Ngara watanufaika vipi na hii asilimia 0.3 ya service levy. Kwa hiyo, naomba nipate maelezo ya kuridhisha kutoka kwa Serikali kwanza kwanini wameamua kutowezeka refinery ifanyike pale pale Ngara. Pili, tutakapokuwa tunabeba haya madini na kuyasafirisha mpaka Kahama ni hasara gani ambayo itatokea katika uharibufu wa barabara zetu. Tatu, wananchi wa Ngara watanufaika vipi kutoka kwenye ile similia 0.3 ya service levy ambayo sasa italipwa Kahama.

Mheshimiwa Spika, labda Serikali ije na mpango madhubuti wa kuhakikisha kwamba Wilaya ya Ngara itapata asilimia fulani kutoka kwenye ile asilimia 0.3 ya service levy. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi nisiporidhika na majibu ya Serikali nitashika Shilingi ya mshahara wa Waziri. Ahsante. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii. Naomba nianze kwa kusema naunga mkono Maazimio yote mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Sekta ya Asasi za Kiraia ambazo mimi ni mwakilishi wao hapa Bungeni kupitia nafasi ya Viti Maalum Chama cha Mapinduzi, napenda kuwasilisha pole za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kufuatia kifo cha Hayati Rais Magufuli. Vilevile napenda kuwasilisha salamu za pongezi kwa Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki hii zaidi ya asasi za kiraia 200 kutoka Bara na Zanzibar zimewasilisha tamko la pamoja la pongezi na pole kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Vivyo hivyo, Jukwaa la Wanawake Wakurugenzi wa Asasi za Kiraia kwa maana ya CSO’s and NGO’s na wao pia wametoa tamko la pongezi kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kupitia Bunge lako Tukufu kuwa Sekta ya Asasi za Kiraia zina imani kubwa sana na yeye kwa sababu ana uzoefu mkubwa sana wa uongozi. Nitumie fursa hii kutaja maeneo machache. La kwanza, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alianza ajira yake kwenye mwamvuli wa mashirika yasiyo ya Kiserikali linaloitwa ANGOZA (Association For Non- Governmental Organizations in Zanzibar) na kwa mantiki hiyo Mheshimiwa Rais ni mwana Azaki mwenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ana uzoefu mkubwa katika masuala ya uwezeshaji kiuchumi. Kupitia uzoefu huu mwaka 2016 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bani Ki Moon alimteua Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan akiwa Makamu wa Rais kuwa Mjumbe wa Jopo la Dunia kama mwakilishi wa Afrika lililopewa jukumu la kumshauri kwenye masuala ya uwezeshaji wanawake kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, miaka 25 iliyopita Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan akiwa anatokea Sekta ya NGO’s alishiriki katika Mkutano wa Beijing uliokuwa unalenga kuleta ukombozi wa usawa wa kijinsia ikiwemo wanawake kwenye nafasi za uongozi na maamuzi. Hivyo kupitia yeye kuwa Rais wetu wa kwanza mwanamke, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameiwezesha Tanzania kuweka historia ya kuwa sehemu ya utekelezaji wa Maazimio ya Beijing. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia, nikiwa kama mdau wa lishe, sisi wadau wa lishe tunatambua juhudi kubwa ambazo Mheshimiwa Makamu wa Rais mteule ameweka katika kuhakikisha nchi yetu inaboresha hali ya lishe. Vivyo hivyo, tunatambua pia jitihada kubwa ambazo Makamu wa Rais mteule, Mheshimiwa Dkt. Phillip Mpango ambazo pia ameweka katika eneo hilo la kuboresha hali ya lishe kwa kuhakikisha kwamba Halmashauri zote nchini zinatenga bajeti ya lishe kwa kulingana na idadi ya watoto wenye chini ya umri wa miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Sekta ya Asasi za Kiraia itampa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza dira yake ya maendeleo ya Taifa letu la Tanzania. Naomba nitumie fursa hii kipekee kuomba kuwasilisha ombi rasmi la kukutana naye kama Sekta ya Asasi za Kiraia ili nasi pia tuwe sehemu ya mafanikio yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamuomba Mwenyezi Mungu aendelee kumbariki na kumlinda Rais wetu, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika, ahsante. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Nami ningependa nijielekeze katika kuhakikisha namna ya kuipunguzia Serikali gharama; kwasababu kwa siku mbili hizi tumesikia michango mingi sana ya Waheshimiwa Wabunge ambayo yote inalenga kuboresha hali ya uchumi wetu na kuboresha pia hali ya maendeleo ya Taifa. Lakini ili Serikali iweze kutimiza yote hayo Serikali inahitaji fedha, Serikali inahitaji Bajeti. Kwa hiyo mimi ningependa kuishauri Serikali, ifike mahala sasa iangalie suala zima la idadi kubwa ya mahabusu walio gerezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwasababu hivi sasa Tanzania ina takribani wafungwa 16,836, lakini vivyo hivyo ina maabusu 16,703 ambapo Jeshi la Magereza kila mwezi linatumia takribani milioni 900 kwa ajili ya kuwalisha hawa wafungwa pamoja na mahabusu; sasa hii ni gharama kubwa sana kwa Serikali. Nasema ni gharama kubwa sana kwa Serikali kwasababu Jeshi la Magereza halina vyanzo vya mapato ilhali linajitegemea. Kwa hiyo binafsi kwanza ninafarijika sana kwamba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Mwigulu Nchemba alikuwa Waziri wa Katiba na Sheria kwa hiyo jambo hili analifahamu fika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile hata katika hotuba za hivi karibuni za Mheshimiwa Rais Mama yetu mpendwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameongelea pia suala la idadi kubwa ya mahabusu gerezani. Sasa tupate picha kidogo ikiwa tutaweza kupunguza idadi ya mahabusu gerezani, ina maana kati ya ile milioni 900 kila mwezi…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Neema kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, ni taarifa ndogo tu. Katika mchango wake amesema Waziri wa Fedha alikuwa Waziri wa Katiba na Sheria, napenda tu kumjulisha kwamba alikuwa pia Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwenye hilo eneo u- concentrate vizuri kuishauri Serikali, ahsante (Makofi).

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Neema endelea na mchango wako.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru lakini pia naomba unilindie muda wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa mantiki hiyo ile milioni 900 ambayo Jeshi la Magereza inatumia kila mwezi kwa ajili ya kulisha chakula wafunga na mahabusu tukiweza kupunguza idadi ya hawa mahabusu ina maana kuna kiasi kikubwa cha fedha ambayo tutaweza kuokoa; na kiasi hicho kila mwezi kitaweza kwenda kufidia kiasi kikubwa cha fedha ambacho kinahitajika ili kutekeleza mipango mbalimbali na ushauri mbalimbali ambao wametoa Waheshimiwa Wabunge ndani ya hizi siku mbili. Kwa hiyo mimi ningependa kuchukua fursa hii kuishauri Serikali ichukue maamuzi madhubuti kabisa ya kuona namna gani tutapunguza idadi ya mahabusu kule gerezani kwa lengo kubwa la kuchangia kupunguza gharama kwa Serikali. Kwasababu mimi ninaamini tunavyochangia mpango lazima pia tuangalie tunaipunguziaje mzigo Serikali, tunaokoaje fedha za Serikali ili zielekezwe huko kunakostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi naona huu ni upotevu wa fedha usio wa lazima. Kwa hiyo pamoja na ushauri huo pengine njia nyingine ambayo tunaweza tukafanya Mahakama ibebe jukumu la kugharamia hii bajeti ya kulisha hawa mahabusu wako gerezani kwasababu kimsingi wako kutokana na ucheleweshaji wa wao kuhakikisha kwamba kesi zote hizi zinafikia kupata hukumu. Na kwa mantiki hiyo hiyo pengine hata na Jeshi la Polisi pia linajukumu katika hili; kwasababu ni kuendelea kuionea Jeshi la Magereza ilhali Serikali imesema ijitegemee na Jeshi la Magereza halina mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi binafsi nina imani kubwa sana atakapokuja kuwasilisha hapa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, ukizingatia, kama alivyosema dada yangu pale kwamba alikuwa ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi alikuwa pia ni Waziri wa Katiba na Sheria basi atatueleza ni namna gani Serikali inapanga kwenda kupunguza idadi ya mahabusu ili ile bajeti ambayo inatumika hivi sasa iende kwenye mambo ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo naomba kuunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nitajielekeza katika maeneo mawili ya lishe na sekta ya Asasi za Kiraia (NGOs).

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Serikali kwa jitihada kubwa ambayo imekuwa inaendelea kufanya katika kuboresha hali ya lishe nchini pamoja na kutokomeza udumavu na aina zote za utapiamlo. Kipekee kabisa napenda kutambua jitihada kubwa alizofanya Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan, akiwa Makamu wa Rais ambayo ilisababisha yeye kumuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kusaini mikataba ya lishe kwa niaba yake na Wakuu wa Mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo, nawashukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa namna ambavyo wanaendelea kuratibu masuala ya lishe ambayo yanaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu. Wanafanya hivi kwa kupitia maeneo matatu. La kwanza ni kusimamia utekelezaji wa mpango jumuishi wa lishe wa Kitaifa; la pili ni kusimamia vuguvugu la uongezaji kasi ya kuboresha hali ya lishe duniani; la tatu ni kujumuisha jumbe ya lishe katika jumbe za mbio za Mwenge wa Uhuru; na la nne latika kutekeleza viapumbele vya lishe vilivyoweka katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kipekee kabisa napenda kukishukuru Chama changu, Chama Cha Mapinduzi kwa kuwa chama pekee ambacho kimeweka kipaumbele kikubwa katika lishe. Mnaweza mkarejea kurasa za 7, 40, 139-141 ambapo Chama Cha Mapinduzi kimeweka malengo madhubuti ya namna gani itaelekeza Serikali kwenda kuboresha hali ya lishe nchini na kutokomeza udumavu na aina zote za utapiamlo. Waheshimiwa wanaweza kurejea Zaidi kwenye kurasa hizi nilizozitaja, kurasa za 7,40, 139-141. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa Tanzania tuna changamoto kubwa sana ya lishe duni inayosababisha kutuweka katika hatari ya kutokuwa na kizazi na nguvu kazi shindani. Wengi humu tunaongelea changamoto za ajira, lakini ikiwa watoto wetu wana lishe duni na wako dumavu hiyo nguvu kazi na kizazi cha kesho tutavipata vipi? Ndiyo maana ni lazima kutoa kipaumbele kwa ajenda hii ya lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kuikumbusha Ofisi ya Waziri Mkuu itamke rasmi ina maoni gani kuhusu janga hili la lishe bora. Ofisi ya Waziri Mkuu itakwenda kufanya nini kuhakikisha kwamba sekta na Wizara zote zinazohusika na suala hili wanakwenda kutekeleza yale yaliyoandikwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo langu la pili la Asasi za Kiraia; napenda kuipongeza sana Serikali kwa wito wa utashi wa kushirikiana na sekta binafsi ili kukuza ustawi wa maendeleo ya jamii na uchumi wa Taifa letu. Hata hivyo, naomba nitumie fursa hii kuikumbusha Serikali kuwa kuna sekta nyingine ambayo nayo inaweza kuchangia katika maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba kuitambulisha Sekta ya Asasi za Kiraia kwa maana ya NGOs, CSOs na CDOs kwa sababu sekta hii ina sifa zote za kuwa chachu ya kuinua na kukweza dira ya mipango ya maendeleo ya Taifa. Nasema hivi kwa sababu hata kwenye Ilani hii ya Chama Cha Mapinduzi imetambua mchango mkubwa wa sekta ya Asasi za Kiraia, imetambua sekta ya Asasi za Kiraia ni muhimu katika kutekeleza mipango ya maendeleo. Mnaweza mkarejea kurasa za 124 na 128 na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo, Chama Cha Mapinduzi ndicho chama pekee ambacho katika nafasi zake za Viti Maalum, kimetenga nafasi ya kuwa na Mwakilishi wa kundi la Asasi za Kiraia. Humu Bungeni niko mimi nikiwakilisha kundi la Asasi za Kiraia kwa upande wa Tanzania Bara, lakini pia yupo Mheshimiwa Khadija Aboud anayewakilisha kundi hili kutoka Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, napenda kuipongeza Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa NGOs kwa kazi kubwa inayofanya kusimamia utekelezaji wa Sheria ya NGOs ya 2019 na kwa mara ya kwanza imeweza kuchakata na kubainisha ni kiasi gani cha fedha kinachoingia nchini kwa ajili ya sekta hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipindi cha miezi sita tu kati ya Julai, 2020 mpaka Machi, 2021, jumla ya mikataba 178 ilichakatwa na kufanyiwa upembuzi na Ofisi ya Msajili wa NGOs. Iliweza kubaini jumla ya shilingi bilioni 546, narudia; katika kipindi cha miezi sita, Ofisi ya Msajili wa NGOs iliweza kubaini jumla ya 546,758,508,000 ziliingia nchini kupitia NGOs. Kwa hiyo moja kwa moja sekta ya NGOs ina mchango mkubwa sana katika kuendeleza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mantiki hiyo, nitumie fursa hii kuiomba Serikali itenge bajeti ya kutosha kwa Ofisi ya Msajili wa NGOs na Baraza la Taifa la NGOs ili waendeleze kusimamia utekelezaji na uratibu katika sekta hii muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo, naomba nikiri kwamba awali nilikuwa na hofu juu ya maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto kumezwa na afya, lakini namshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa kulitambua hilo na kuweka Naibu Waziri anayesimamia Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa ajira, Sekta ya Asasi za Kiraia inaajiri watu wengi. Kwa taarifa ya Wizara ya Afya, 2017, katika mashirika 300 tu yalichangia zaidi ya ajira 5,317. Vile vile sekta hii ya Asasi za Kiraia pia ni tanuru ya kuandaa viongozi wa Kitaifa. Viongozi hawa wa Kitaifa ni kuanzia Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan; Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa; Mheshimiwa Waziri, Profesa Kabudi; Mheshimiwa Waziri, Profesa Kitila Mkumbo; Mheshimiwa Waziri, Ummy Mwalimu; Mheshimiwa Waziri, Selemani Jafo; Mheshimiwa Naibu Waziri, Olenasha; Mheshimiwa Naibu Waziri, Ummy Nderiananga; Mwanasheria Mkuu, Mheshimiwa Profesa Kilangi. Kwa hiyo hii moja kwa moja inaonesha kwamba sekta hii inatoa mchango mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitumie fursa hii kuiomba Serikali, vile ilivyowakaribisha sekta binafsi waandae mpango kazi na sisi pia sekta ya Asasi za Kiraia tupewe fursa kama hiyo tukaribishwe rasmi, maana tupo tayari kushirikiana na Serikali na tayari tunaandaa mpango kazi ambao tutapenda kuuwasilisha kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa, kabla ya kwenda kumwona Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan, kama ambavyo nilishaomba awali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia, ndani ya Bunge hili tuko Wabunge wengi sana ambao tumepitia sekta ya Asasi za Kiraia. Hivyo, naona tunayo fursa ya kuanzisha kikundi cha Wabunge Vinara wa AZAKI kwa maana ya NGOs, CBOs na CSOs ili kuimarisha utekelezaji wa mwongozo, uhusishwaji wa Asasi za Kiraia katika shughuli za Kamati ya Bunge na huu ni mwongozo ambao umeandaliwa na Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Nashukuru sana kwa fursa hii. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami napenda niungane na Wabunge wenzangu kuipongeza sana Serikali kwa bajeti nzuri na bajeti ya kimkakati ambayo inakwenda kuinua wananchi wote hususan wananchi wa chini. Kipekee kabisa napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kasi ambayo amekuja nayo na nia yake ya dhati ya kuhakikisha kwamba maendeleo yanawafikia Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo mimi napenda nichangie kwenye eneo la vyanzo vipya vya mapato, hapa nitaanza na eneo langu la kwanza ambalo linahusu huduma ya sekta hii ya ki-digital kwa mujibu wa takwimu za TCRA Tanzania ina jumla wa watumiaji wa Internet Milioni 29 lakini vile vile ina jumla ya watumiaji wa huduma za kupokea fedha kwa njia za mtandao wa simu Milioni 32 hivyo hii sekta ya ki-digital ni sekta kubwa na ninaipongeza sana Serikali kwa kutambua hilo na hata kuunda Wizara mpya ambayo ina dhamana ya masuala mazima ya TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningependa kumshauri Waziri na Serikali kwa ujumla ifanye mapitio ya Sheria ya Kodi ya Mapato ya mwaka 2004 pamoja na Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani ya mwaka 2014 ili sheria hizi mbili ziweze kuwa na vifungu vitakavyowezesha utozwaji wa kodi kwenye biashara ya sekta hii, napendekeza Serikali ije na kodi ya huduma za ki-digital kwa maana ya digital service tax nasema hivi kwa sababu hivi sasa kuna huduma nyingi zinafanywa na sekta hii ambazo chanzo chake ni ardhi ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwakuwa chanzo chake ni ardhi ya Tanzania basi Serikali inayo fursa ya kutoza kodi aina ya digital service tax nitatoa mfano mdogo, matangazo ya biashara yanayofanywa kupitia online platforms yaani mitandao ya kijamii kama Facebooks, Instagram, Twitter Google nayo yanaweza kuwa ni fursa ya kutozwa kodi, vilevile yapo masoko ya kimtandao ambayo yanakutanisha wanunuzi na wateja kama Amazon, E-bay, Alibaba, Kikuu na kadhalika, nako kunaweza kukawa kuna fursa ya kutoza kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia zipo biashara za kukodi usafiri na hoteli kama vile wengi tunatumia Uber, Boat, Airbnb booking.com nayo ni fursa ya Serikali ya kutoza kodi, lakini pia lipo eneo hili la michezo ya kubahatisha yaani online betting. Nimeona Serikali imependekeza kushusha ile gaming tax on winning kutoka asilimia 20 kwenda asilimia 15 lakini kiuhalisia wengi wanapenda kutumia online betting kwa sababu unapocheza online betting hakuna kodi ambayo unalipia kwa hiyo nayo hiyo ni fursa ya Serikali kutoza kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuikumbusha Serikali kwamba hivi sasa tunao kakribani Watanzania Millioni 5.9 ambao wanatumia mitandao hii ya kijamii. Hivyo kwa mantiki hiyo, ninaiomba sana Serikali iiangalie sekta hii kwa jicho la kipekee na ije na utaratibu wa kutoza kodi ambayo inaweza ikaenda kwa jina la digital service tax ili kuhakikisha kwamba Tanzania tunanufaika na sekta hii ambayo inakua, ambayo inaendana na digital economy na hata Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii ya masuala ya TEHAMA aliahidi kwamba ataandaa sera ya digital economy, kwa hiyo kwa ujumla wake nadhani tutapata fursa ya kupata vyanzo vipya vya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la pili napenda kuongelea nishati ya jua, nafahamu kwenye Bunge lililopita Bunge la 11 Bunge lako Tukufu mlipitisha kuweka msamaha wa kodi wa ongezeko la thamani kwenye vifaa vya nishati ya jua (solar) lakini kwenye mapendekezo ya Mheshimiwa Waziri, amependekezwa kwamba afute msamaha huu, na hii inaendana na ile unpredictability ya sera zetu, nasema hivi kwa sababu Serikali imefanya jitihada kubwa sana ya kuhakikisha kwamba umeme unafika mpaka vijijini, lakini mpaka sasa tunavyoongea kuna vijiji takribani 2000 bado havina umeme na hata vijiji ambavyo vina umeme, umeme umefika kwenye centre sio kaya zote zenye umeme na sio vitongoji vyote kwa hiyo bado wananchi wetu wanategemea kwa kiasi kikubwa umeme unaotokana na solar nishati hii ya jua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule vijijini ukienda wanategemea solar kwa ajili ya Zahanati, wanafunzi wanategemea solar kwa ajili ya kusomea, wananchi kule wanategemea solar kwa ajili ya kupata habari, wanategemea solar kwa ajili ya kuchaji simu zao. Mheshimiwa Waziri hili pendekezo la kuondoa ule msamaha wa kodi kitakachokuja kutokea ni kwamba gharama ya kupata vile vifaa vya solar itaongezeka kwa takribani asilimia 27 mpaka asilimia 35 na ambaye atakwenda kuumia kwenye gharama hii ni yule mtumiaji mwananchi wa kijijini ambaye Serikali ya Awamu ya Sita, Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan Rais wetu anataka kuhakikisha kila mwananchi popote pale alipo aweze kupata maendeleo na maendeleo ya kiuchumi chachu mojawapo kubwa ni nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi ninaiomba sana Serikali kwa unyenyekevu mkubwa wauache huu msamaha wa kodi kwenye eneo hili uendelee kubaki pale pale kwasababu kuiondoa kuifuta ni kumuumiza mwananchi wa chini ambaye Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ndiye anayemtetea na ndiye anaye mpigania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la mwisho ni eneo la lishe napenda tu kusema kwamba, nadhani wakati umefika sasa Serikali iweke jitihada kubwa zaidi na uwekezaji kwenye kinga badala ya tiba, nasema hivi kwasababu kwa taarifa za Serikali kama tutaendelea Tanzania kuwa na hali ya ukosefu wa lishe bora tuliyonayo kwa kipindi cha miaka 10 yaani tangu 2014 mpaka 2025 Taifa letu litapoteza mapato mengi sana kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwaka tutakuwa tunapoteza Trilioni mbili kwasababu ya kuwa na hali ya udumavu tuliyonayo, kila mwaka tutapoteza Bilioni 230 kwa sababu ya upungufu wa damu kwa wanawake wajawazito, kila mwaka tutapoteza Billioni 15 kwa sababu ya upungufu wa madini joto, lakini kama hiyo haitoshi napenda niongezee kwamba tutakapokuja kwenye yale magonjwa yasiyoambukiza, ambayo yanamahusiano na lishe kama kisukari, moyo, pressure, figo, Inni na aina mbalimbali za cancer kwa taarifa za Serikali inasema kwamba kila mwaka Tanzania inatumia bilioni 457 kugharamia magonjwa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na magonjwa haya yanapelekea hata mfuko wetu wa Bima ya Taifa upo taabani sasa basi, na kama hiyo haitoshi hivi sasa Tanzania inakadiriwa kila mwaka asilimia 2.65 ya pato ghafi la taifa yaani GDP linapotea tu kwasababu ya udumavu. Sasa kama kila mwaka udumavu tu unachangia pato ghafi letu la Taifa lipungue kwa asilimia 2.65, mimi nadhani wakati umefika na Mheshimiwa Waziri pamoja na wachumi wabobezi kabisa ambao tunao ndani ya Wizara watakubaliana nami kwamba wakati umefika Serikali iweke jitihada kwenye kinga badala ya tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningependa kupendekeza yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kwamba sera ya chakula na lishe imeshakamilika imebaki tu kupitishwa na sera hii ipo kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu naomba sera hii kwa heshima zote na unyenyekevu ifanyiwe kazi, lakini pia napenda kupendekeza Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango ione namna ya kuja na kodi ndogo kwenye vyakula ambavyo vina sukari nyingi, mafuta mengi na chumvi nyingi, hii itamlinda mlaji lakini pia itaipatia Serikali pato zuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono ….

NAIBU SPIKA: Hebu ngoja kwanza umesema kwenye chakula chenye sukari nyingi, mafuta mengi wachaji kodi ndogo.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nchi za wenzetu walichofanya hasa nchi za Bara la Ulaya ili kupunguza kasi ya magonjwa yasiyo ambukiza wametambulisha kodi kwa mfano wenyewe wanaiita sugar tax kwa hiyo kama juisi ambazo zimewekwa kiwango kingi sana cha sukari basi inatozwa.

NAIBU SPIKA: Sasa umetumia neno kodi kidogo hapo ndiyo tumepata changamoto.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kodi kubwa.

NAIBU SPIKA: Haya ahsante.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nashukuru. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii nami nichangie na mchango wangu utajielekeza kwenye taarifa ya Kamati ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa maana ya PIC.

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza zaidi kwenye Bima za Ndege (Aviation Insurance) za Shirika letu la ndege la ATCL. ATCL imekuwa ikikata bima za ndege zetu kupitia Shirika la Bima la Taifa NIC, ambao nao wamekuwa wakikata bima kwa kupitia kampuni ya nje (International Broker) inayojulikana kwa jina la MASH. NIC wamekuwa wakifanya hivyo. Kwa kutumia mfumo wa single source. Sasa kwa ufupi, kila mwaka Shirika la ATCL limekuwa likilipa bima ya gharama ya ndege zake, zifuatazo, nanukuu: -

“Mwaka 2018/2019 Bima ya Afya kwa mwaka ilikuwa takribani Shilingi bilioni 5.8; kwa mwaka 2019/2020, gharama ya bima kwa mwaka ilikuwa takribani Shilingi bilioni 14.5; kwa mwaka 2020/2021 gharama ya bima kwa mwaka ilikuwa takribani Shiligni bilioni 18.7 na kwa mwaka 2021/2022 gharama ya hizi bima za ndege ilikuwa takribani Shilingi bilioni 21.3.”

Mheshimiwa Spika, sasa kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023, Shirika la ATC liliamua kuitaka NIC walete kampuni nyingine ambazo zinaweza zikatoa huduma hii ili kufanya ulinganifu wa gharama ya bima kila mwaka ambayo Shirika la ATC wanalipia. Walipofanya zoezi hilo, waliweza kupata kampuni mbadala inayojulikana kwa jina la WILL STAWA, ambao walitoa quotation ambayo ilikuwa ni pungufu ya gharama ya yule international broker ambaye NIC anamtumia siku zote kwa takribani Shilingi bilioni tatu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kitendo hicho, Shirika la Bima la Taifa la NIC lilisababisha yule single source, International Broker wanayemtumia (MASH) naye akashusha quotation yake kwa gharama ya Shilingi bilioni tatu ili ifikie ile ya kati ya hao wapya ambao walikuwa wamejitokeza. Jambo hilo binafsi naona lina utata kidogo, inakuwaje kwa urahisi tu uweze kushusha kwa zaidi ya takribani bilioni tatu kwenye bima za ndege kwa mwaka?

Mheshimiwa Spika, ili Shirika la Bima la Taifa (NIC) liweze kukidhi Matakwa ya Sheria ya Manunuzi ya Umma inatakiwa yule international broker awe na partner wa hapa Tanzania. Kwa hiyo, ndivyo ambavyo wameendelea kuwa wanafanya hivyo. Yule partner wa Tanzania anapata 15% ya premium commission, lakini ikifanyika tafiti vizuri, inaonekana kwamba yule local partner ambaye ameandikwa yupo tu kwenye makaratasi, haonekani katika uhalisia. Jambo ambalo nalo linatiliwa shaka na inatakiwa tuliangalie kwa umakini.

Mheshimiwa Spika, kwa nyongeza, nimefanya tafiti ndogo kujaribu kulinganisha gharama ya bima za ndege zetu ambazo ATCL inalipa, kwa kulinganisha na gharama za bima za kila mwaka ambazo Mashirika ya Ndege ya Nchi za Afrika Mashariki wanalipa. Takwimu hizo ni kama ifuatavyo: -

(i) Kenya Airways wana ndege 39 na gharama ya bima kwa mwaka ni dola za Kimarekani ni milioni 9.7 kwa ndege 39;

(ii) Rwandan Airways wana ndege 12 na gharama ya bima kwa mwaka ni dola za Kimarekani milioni 2.8; na

(iii) Shirika letu la Air Tanzania lina ndege 11, lakini gharama ya bima kwa mwaka ni dola za Kimarekani 5.9.

Mheshimiwa Spika, kwa hesabu za haraka haraka, unaona jinsi gani ambavyo Shirika letu la Ndege la Tanzania (ATCL) linalipa gharama kubwa kwa mwaka, kwa ajili ya bima za ndege ambayo haiendani na uwiano, yaani ukilinganisha na idadi ya ndege zilizopo na hii ni kwa kulinganisha na wenzetu wa nchi jirani kwa maana ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, bima za ndege kwa sasa hivi mkataba uliopo unakwenda mpaka mwezi Juni, 2023. Kwa hiyo kwa unyenyekevu mkubwa naomba kupendekeza kwamba, tuongeze nyongeza ya azimio katika mapendekezo ya Kamati hii husika, kuielekeza ATCL ifanye competitive tender zabuni kwa ushindani ili kuhakikisha kwamba tunakwenda kuokoa fedha za Serikali na umma. Maana hata taarifa ya Kamati imesema kwamba ATCL iko taabani kiuchumi. Sasa kama iko taabani kiuchumi wakati kwa upande mwingine tunalipa gharama kubwa kuliko inavyotakiwa kwenye gharama ya kila mwaka ya bima kwa ndege, hapo tunatakiwa tufanye jambo sisi kama Bunge ili kuhakikisha kwamba tunaokoa fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko pia suala la local content, ambalo hata Mheshimiwa Rais Samia Hassan, amekuwa akilisemea kwa mara nyingi na ushiriki wa sekta binafsi kwa Tanzania. Sasa Shirika la Bima la Taifa (NIC) hivi sasa ni kama lina monopoly. Kutokana na monopoly hiyo, NIC inakuwa na mamlaka ya kuamua kutumia single source international broker. Single source huyo pale ambapo inaelekea anaweza akatokea mbadala mwenye gharama ya chini, amepunguza kwa urahisi bilioni tatu kwenye quotation yake. Jambo ambalo naomba kwa unyenyekevu mkubwa tuone namna ya kuishauri ATCL, ihakikishe inatangaza zabuni za bima za ndege kwa kutumia ushindani na sio single source, kwa sababu single source inaweza ikapelekea mianya ya upotevu wa fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wabunge, tunao wajibu wa kuhakikisha jitihada za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan za kutafuta fedha na fursa mbalimbali kwa ajili ya nchi yetu na Watanzania hazififishwi kwa mianya hii ya single source. Kwa unyenyekevu mkubwa, naomba tutoe pendekezo hili la kuhakikisha kwamba zabuni za bima za ndege za ATCL zifanyike kwa competitive bidding.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, ni matumizi ya TEHAMA. Hili nalo ni eneo ambalo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akilisemea kwa nguvu kubwa. Nimejaribu kutafakari katika uwekezaji wa miradi yetu mikubwa hapa Tanzania, nikifanya rejea kwenye SGR pamoja na mradi wa kufua umeme wa Mwalimu Nyerere, ukifanya tathmini ya kujua ni makampuni mangapi ya Kitanzania ambayo yamepata zabuni za TEHAMA kwenye miradi ile, majawabu yake ni ya kusikitisha sana. Pia ukitaka kufahamu ni wataalam wangapi wa TEHAMA wa Kitanzania ambao wamepata nafasi ya kufanya na wenzetu wa nje waliopata zabuni hizo ili waweze kupata kile kitu tunachokiita transfer of knowledge, nayo utasikitika sana.

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo, naomba nitoe angalizo kwamba, kwenye miradi yetu mikubwa ya kimkakati, tunapotoa zabuni za TEHAMA kwa makampuni ya nje, tunajiweka katika hatari ya kiusalama wa mfumo. Suala la TEHAMA ni suala nyeti. Kwa mfano, ile kampuni ikiamua kuzima mtambo, sisi kama nchi tutafanyaje? Wakati hatutumii watalaam wetu wa ndani?

Mheshimiwa Spika, nikirejea kwenye suala la Sensa. Tumekwishajidhihirisha kupitia sensa. Shirika la Takwimu la Taifa limetumia wataalam wetu wa ndani na sensa yetu imeendeshwa kidigitali mpaka watu wa Mataifa ya nje wametusifia. Kwa hiyo, tunao uwezo wa kutumia wataalam wetu wa ndani.

Mheshimiwa Spika, tutoe maelekezo mahususi kuhusu Serikali kuweka jitihada pale ambapo kuna miradi ya kimkakati, hususani masuala ambayo yanaendana au yanaweza kupelekea masuala ya kiusalama, tuweke mbele kuhakikisha kwamba tunatafuta Makampuni ya Kitanzania ambayo yanaweza kutekeleza ile kazi au Makampuni ya Kitanzania yashirikiane na makampuni ya nje ili kulinda maslahi letu likiwemo suala la kiusalama.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, kwa unyenyekevu mkubwa, nashukuru sana kwa fursa hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza kabisa, napenda kuipongeza Serikali kwa kuja na Sera ya Elimu bure na uwekezaji mkubwa katika miundombinu. Napenda niseme kwamba, kama tutaendelea kutotilia maanani suala la lishe shuleni, jitihada hizi zote zipo hatarini.

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu mtoto anapokuwa darasani lazima aweze kufikiri, kuelewa, kuchakata na kukariri kile anachofundishwa na mwalimu; lakini kama ubongo wake haufanyi kazi vizuri, kama ubongo wake haujapata virutubisho sahihi, basi mtoto huyu hawezi kujifunza ipasavyo na hiyo ni sawa sawa na kutegemea gari lisilo na mafuta liweze kutembea.

Mheshimiwa Spika, wanafunzi wanatoka nyumbani alfajiri, wengi wanakuwa hawajala, wanakwenda shule wanashinda njaa, akiwa darasani tumbo linanguruma, tumbo linanguruma kwa sababu linakosa kitu cha kusaga na kupeleka kwenye ubongo. Kwa hiyo mwanafunzi anakosa umakini kiasi kwamba Mwalimu anaweza kutoka kufundisha, ukamuuliza mwanafunzi mwalimu kasema nini akasema sijui. Mtoto yule ukahangaika kumpiga na kusema kwamba ni mtukutu, hana adabu, hasikilizi darasani lakini kumbe ubongo wake uli-cease kufanya kazi kwa sababu ya njaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ningependa kuikumbusha Serikali kwamba pia hali ya udumavu nchini inachangia kwa kiasi kikubwa kwa watoto kutoweza kufaulu na kufundishika shuleni. Wenzetu wataalam wa lishe TAMISEMI wanatuambia kwamba katika kila darasa la watoto 45, watoto 15 hawafundishiki. Sasa tupate picha tuna jumla ya wanafunzi milioni 11, kama katika kila 45 15 awafundishiki ina maana pamoja na jitihada zote hizi tunaendelea kufifisha hizi jitihada kutokana na uwelewa na ufaulu ndio maana unakuwa huko chini. Kwa hiyo naiomba Serikali iweke mikakati madhubuti ya kuhakikisha kwamba kila shule hususani za kutwa pia wanazalisha mazao yenye lishe kwa mfano viazi lishe, maharage lishe, mahindi lishe na mengineyo ili kuhakikisha kwamba watoto hawa hawashindi shuleni wakiwa na njaa.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kusema kwamba pamoja na jitihada zote za elimu bure pamoja na jitihada zote za miundombinu bora, ikiwa bado tutaliweka pembeni suala la lishe shuleni jitihada hizi zote zitafifisha malengo ya Serikali ya kuhakikisha kwamba elimu yetu inanufaisha watoto wa kitanzania. Kwa hiyo naiomba sana Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ije na mkakati madhubuti tunakwenda kufanya nini ili kuhakikisha watoto wanapata lishe shuleni.

Mheshimiwa Spika, eneo langu la pili ni upande wa hedhi salama. Naipongeza sana Serikali kwa mikakati mbalimbali iliyowekwa kuhakikisha mtoto wa kike anabaki shuleni, kuhakikisha kwamba mtoto wa kike analindwa ili apate elimu. Hata hivyo, mtoto huyuhuyu wa kike kila mwezi anapofika umri wa kubalehe anakosa siku tano mpaka siku saba kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi. Kwa hiyo suala hili pia naiomba Serikali ilitilie mkazo. Nafahamu kuna bajeti ndogo kwenye elimu bure ya kupata msaada wa taulo za kike kwa dharura lakini Serikali iweke wazi kwa sababu dharura zinakuwa nyingi, lakini pia Serikali ije na mkakati madhubuti katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano mdogo tu, kwenye shule za msingi kuna wanafunzi wa kike 5,481,982; kwenye shule za sekondari kuna wanafunzi wa kike milioni 1,284,410; kati ya hawa wote tukichukulia tu asilimia 20 wako kwenye umri wa kubalehe ina maana tuna jumla ya watoto milioni 2,380,806 ambao kila mwezi wako hatarini kukosa shule siku tano mpaka siku saba. Hili ni jambo zito sana ambalo Wizara inabidi iliangalie kwa jicho la kipekee. Wale ambao wanakwenda shule, wanatumia vitu ambavyo ni hatari sana kwa afya zao, wanatumia mabanzi, wanatumia magazeti, wanatumia vitu ambavyo vinapelekea na naamini kwamba vinachangia kwa ongezeko kubwa la kansa ya shingo ya kizazi. Kwa hiyo naiomba sana Serikali ione namna gani itaweza kusaidia na kuhakikisha kwamba mtoto wa kike hakosi shule kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia naamini kwa sababu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia ni mama yetu Profesa Ndalichako na haya masuala yote mawili lazima yanamgusa moja kwa moja kama mama, naamini kabisa atakuja na mpango madhubuti wa kuhakikisha moja watoto wanapata lishe shuleni, lakini pili, mtoto wa kike hakosi shule kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Kwanza kabisa natoa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa mwongozo na nia yake ya kuhakikisha miundombinu ya teknolojia ya mawasiliano inafika asilimia 80 ifikapo mwaka 2025. Haya ni maono makubwa ambayo yatatupelekea kuimarisha uchumi wetu zaidi. Eneo la teknolojia ya mawasiliano ni sekta mpya ambayo ikiangaliwa kwa umakini, nchi hii inaweza kujipatia kipato kikubwa pamoja na kutengeneza ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mdogo kwa ndugu zetu Wakenya, sekta ya teknolojia ya mawasiliano inachangia asilimia nane ya pato ghafi la Taifa; na tayari sekta hii kwa Kenya imeshatengeneza kakribani ajira 250,000; na hii ni kwa takwimu ya Serikali ya Kenya. Ukuaji wa sekta ICT Kenya umepita ukuaji wa sekta zote kwa zaidi ya asilimia 23 na hii ni kwa mlongo uliopita peke yake. Kwetu hapa Tanzania bado kuna changamoto ambazo tukiziangalia vizuri zitasaidia kuongeza ajira katika sekta hii ambayo hivi sasa tumeifunga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe tu mfano mdogo, wachangiaji wengi asubuhi waliongelea kuhusu YouTube. Hivi sasa kwa Tanzania YouTube mazingira yake siyo Rafiki. Nasema hivi kwa sababu wako wanamuziki wachache ama wadau ambao wanatumia YouTube kama akina Dimond, Alikiba na Milard Ayo ambao wamenufaika; lakini baada ya kuleta sheria ambazo zimepelekea changamoto, wako pia watu wengi ambao wamejiondoa kutumia mtandao huu ambao wengi wao ni vijana. Sasa hii inaleta changamoto kubwa kwa sababu vijana hawa wanatumia teknolojia hii na sekta hii kujipatia ajira ambazo ni changamoto. Kwa hiyo, sera zetu lazima ziweke mazingira ya kuwawezesha wao kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto hii, tofauti na nchi nyingine, hapa Tanzania vijana wengi ambao wapo kwenye sekta hii hawana elimu rasmi ya masuala ya kidijitali. Kwa hiyo, tunapowaongezea gharama za kulipa ni kufifisha jitihada zao binafsi ambazo wao wenyewe wamezichukua kama viijana kujitengenezea ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naomba niishauri Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia masuala yafuatayo: jambo la kwanza, Wizara ione namna gani itaweza kupunguza gharama zinazolipwa na Watanzania hususan hawa vijana kwa sababu hivi sasa ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, naiomba Wizara ifanye mapitio ya sheria ili kuona namna ya kuondoa baadhi ya makosa kutoka kuwa makosa ya jinai iwe makosa ya madai, kwa sababu na yenyewe inaleta changamoto kubwa sana kuhakikisha kwamba watu wananufaika na sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu, tuongeze ufikiaji wa internet kama ambavyo wengine wamechangia, hususan kule vijijini, hata tukiweza kufikia 3G. Tumeona kwenye miji mikubwa hii access ya internet inasaidia sana kufanya biashara, hususan kwa viijana na wanawake. Ukiingia mtandao wa Instagram, wengi wananufaika sana, lakini fursa hizi hazitunufaishi wale ambao tunatoka hususan Mikoa ya pembezoni. Kwa hiyo, nadhani lazima jitihada zifanyike katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile bado gharama za kupata internet hapa nchini Tanzania ni kubwa ukilinganisha na majirani zetu. Nitatoa mfano mdogo. Nairobi gharama ya uzito kwa mwezi ni Dola za Kimarekani 5.5, tukienda Uganda ni Dola za Kimarekani 10; Uganda kwa maana ya Mji wa Kampala, lakini tukija Tanzania kwa maana ya Mji wa Dar es Salaam ni dola za Kimarekani 15.5. Kwa hiyo, unaweza kuona ulinganishi. Kwa Nairobi ni 5.5 kwa Dar es Salaam 15.5. Kwa hiyo, nadhani ni muhimu tufanye tena uangalizi wa gharama hizi, kwa sababu kwa ilivyo sasa hivi Watanzania wengi hawafaidiki na hawanufaiki na sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kufanya hivyo, tutaipunguzia Serikali mzigo wa ajira kwa vijana, kwa sababu tutaweza kufungua vijana kujiajiri kupitia Sekta hii. Katika hili naomba niishukuru Kamati kwa sababu na wenyewe pia wamelisemea suala hili kwenye wasilisho lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa tano, naomba Serikali iangalie namna ya kushirikiana na wabunifu ili kuongeza faida ambayo inapatikana na sekta hii. Yaani Wizara msijifungie, kwa sababu wako vijana ambao ni wabunifu tuone ni namna gani tunaweza tukashirikiana nao. Katika eneo hili nichukue fursa hii nimpongeze sana Spika, Mheshimiwa Job Ndugai kwa sababu kwa jitihada zake awali alifungua milango akakutana na vijana ambao ni wabunifu hadi wakatengeneza App iliyokuwa inawezesha vijana pamoja na wananchi kuwa karibu na Wabunge wao. Kwa hiyo, huo ni mfano tosha kwamba hata Wizara ikishirikiana na hao wabunifu inaweza ikaleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, nirudie tena kwamba tunaweza tukajifunza kwa wenzetu wa Kenya ambao wana Sera ya Digital Economy Blueprint ambayo hivi sasa sisi Tanzania hatuna. Yote ambayo yamechangiwa hapa, kama tutakuwa hatuna sera madhubuti ya Digital Economy Blueprint, mengi haya yatashindikana kwa sababu hii ni sekta ambayo inahitaji iwe na miongozo thabiti na iwe na njia zote ambazo zitahakikisha zinawalinda watumiaji na walaji wa hii sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuwasilisha, angalau pia atueleze: Je, ana mpango gani wa kuja na Sera ya Digital Economy Blueprint. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa fursa hii, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hoja hii muhimu ya hotuba ya bajeti ya Wizara ya Elimu. Kwanza kabisa natoa pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoleta mageuzi makubwa katika Sekta hii ya Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu katika Bajeti ya Wizara hii ya Elimu, nitajikita katika eneo la lishe na hapa naomba nitambue kwamba eneo la lishe ni moja ya maeneo ya vipaumbele ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan tokea akiwa Makamu wa Rais. Vilevile eneo hili la lishe ni moja ya vipaumbele ambavyo vimeainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, chama changu pendwa ya mwaka 2020 - 2025 ukienda kwenye ukurasa wa saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo, naomba nirejee katika Sera ya Elimu ya Mwaka 2014 ambayo hivi sasa inafanyiwa mapitio. Katika sera hii imeainisha bayana kwamba Serikali itahakikisha inatoa huduma muhimu ikiwemo chakula shuleni. Naamini Serikali ilifanya vile kwa kutambua umuhimu wa chakula na lishe shuleni, lakini kwa bahati mbaya sana utekelezaji wa suala hili umekuwa na changamoto kubwa na hautekelezeki ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kelele nyingi za wazazi pamoja na wadau, niipongeze Wizara ya Elimu ilifanya tafiti na baadaye ikaleta mwongozo. Mwongozo huu hapa ambao ulizinduliwa mwaka 2021 ambao ni Mwongozo wa Kitaifa wa Utoaji wa Huduma wa Chakula na Lishe kwa Wanafunzi wa Elimu ya Msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwongozo huu na kutokana na tafiti iliyofanywa na Wizara ya Elimu, ilibaini kwamba katika shule za kutwa asilimia 70 hazitoi huduma ya chakula na lishe shuleni. Kwa msingi huo nifanye rejea ndogo tu, kwamba kwa takwimu za mwaka 2021 za Serikali shule za msingi ambazo tunazo hapa Tanzania ni takribani 18,546 na jumla ya wanafunzi ambao wako kwenye shule hizi za msingi ni takribani milioni 11.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukijirejea kwenye ile asilimia 70 ya shule zetu hazitoi chakula na lishe shuleni. Kwa muktadha huo inamaanisha kwa mwaka 2021 jumla ya watoto takribani milioni 7.9 walikuwa wanaenda shule wana shinda na njaa na dunia imeshatambua ikiwemo WHO, World Bank na Mataifa ya nje na hata hapa ndani, hapa nchini kwamba chakula na lishe vina mchango mkubwa moja kwa moja katika makuzi ya mtoto pamoja na ufaulu wa darasani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata na wenyewe Wizara ya Elimu wametambua na wameiweka humo kwenye mwongozo ambao wameutoa. Sasa nimejaribu kufanya ulinganifu ambao Wizara ya Elimu inaweza ikafanya tafiti nzuri zaidi na kukokotoa kwa kina zaidi. Matokeo ya mwaka 2022 mwaka jana ya mtihani wa kidato cha nne, asilimia 51 ya wanafunzi wote waliofanya mtihani wa kidato cha nne mwaka jana walipata division four. Asilimia 12 ya wanafunzi wote waliofanya mtihani kwa mwaka 2022 walipata divison zero, ukijumlisha hizi asilimia 51 na asilimia 12, unapata asilimia 63, ambayo haipishani sana na ile asilimia 70 ya shule ambazo hazitoi chakula na lishe shuleni. Kwa hiyo kwa muktadha huo unaweza ukaona kwa tafiti na ulinganifu wa haraka haraka kwamba ni dhahiri pamoja na sababu zingine ukosefu wa chakula na lishe shuleni una mchango mkubwa katika ufaulu wa wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo linalonisikitisha ni kwamba japokuwa kule kwenye Sera ya Mwaka 2014, Serikali imetambua na kusema kwamba Serikali itahakikisha inatoa huduma muhimu katika shule ikiwemo chakula shuleni. Sasa cha kushangaza katika mwongozo huu wa utoaji wa huduma ya chakula na lishe shuleni, Serikali imejivua jukumu hilo na badala yake imeelekeza kwamba utekelezaji wa mwongozo wa chakula na lishe shuleni ni jukumu la jamii na wazazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo linasikitisha kwa sababu, ni Serikali hii hii kwa kutambua uwezo na uchumi hafifu wa wananchi na wazazi uliamua kuja na elimu bure ili kumwondolea mzazi mzigo wa kulipa ada na michango mbalimbali lakini Serikali hii hii kwa kutambua wazazi wale wale, sasa imeamua kuwavika wao jukumu la huduma ya chakula na lishe shuleni na yenyewe ikajiondolea jukumu hilo wakati katika Sera ya Elimu ya 2014, inatambua kwamba hilo ni jukumu la msingi la Serikali. Kwa hiyo jambo hili linahitaji liangaliwe kwa kina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu kuna kitu kinaitwa human capital development, rasilimali watu, kwa Taifa kama la Tanzania kama ambavyo linakua kwa kasi inayokua, kwa uwekezaji mkubwa ambao unafanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan tusipowekeza vya kutosha kwenye hii rasilimali watu yetu tutajikuta huko mbeleni tuko kwenye shida. Kwa hiyo, niombe sana Wizara ya Elimu wanapofanya mapitio ya mitaala pamoja na mipango mingine, tutafute namna ya kuhakikisha ya kwamba suala la chakula na lishe shuleni liwe ni suala la msingi kwa sababu si suala la anasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mapendekezo mawili yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo la kwanza, ninaiomba sana Wizara ya Elimu ichakate namna ambavyo chakula na lishe shuleni kinatakiwa kitolewe, kwa sababu hivi sasa hakuna mwongozo. Huu mwongozo uliotolewa ni mzuri lakini mwongozo katika maneno, hakuna mwongozo ambao unasema hicho chakula na lishe ni cha aina gani? Hicho chakula na lishe wastani wa gharama kwa kila mwanafunzi ni kiasi gani kwa mwezi ili wazazi wajue kwanza ni kiwango gani. Maana yake hivi sasa kila shule inajipangia yenyewe kiwango chake lakini pia lazima kuwe kuna uhakika hicho chakula kinachotolewa kweli kina lishe au ni chakula ili mradi tu kushibisha tumbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa pili. Serikali kupitia Wizara ya Elimu itafute namna ya kutokwepa jukumu lake la msingi la kuchangia na kuhakikisha katika shule zetu kuna huduma ya chakula na lishe, hivyo ichangie katika gharama. Serikali inatoa ruzuku kwenye maeneo mengine kupitia capitation. Kwa hiyo, ninaiomba Wizara ione namna gani ambavyo na yenyewe kulingana na ule mwongozo utakaokuwa umenyambulisha gharama za kila mtoto kupata chakula na lishe shuleni, Serikali ichangie walau asilimia 60 na wazazi wachangie asilimia 40 lakini hiyo ionekane wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa niipongeze sana Serikali kupitia Wizara ya Elimu. Mwaka jana mwezi wa Tisa, Serikali kupitia Wizara ya Elimu wamejiunga na kitu kinaitwa School Meals Coalition. Huu ni mpango wa dunia ambao nchi zinajiunga na moja ya ahadi ambazo wanaweka ni kwamba ifikapo mwaka 2030 kila mtoto katika kila shule atapata walau mlo mmoja wa chakula na lishe kwenye shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa 2030 siyo mbali, hatutaweza kufika kama Wizara ya Elimu itaendelea kutolitilia maanani suala hili na kuanza kuwa na mipango nalo. Kwa hiyo, hapa jambo kubwa ambalo lipo niombe sana Wizara itafute namna ambavyo itapata fedha kwa ajili ya kufanikisha jambo hili na fedha zipo duniani. Yako mashirika ya kimataifa na iko mipango ya kimataifa ambayo tayari inasaidia nchi zingine Barani Afrika kutekeleza ajenda ya chakula na lishe shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo niliwahi kusema katika moja ya michango yangu hapa kwenye bajeti hii hii ni GPE (Global Partnership for Education). Tunayo bahati kubwa kwamba Mwenyekiti wa GPE ni Rais Mstaafu wa Tanzania, Mheshimiwa Dokta Jakaya Kikwete. Sasa tunashindwa nini kutumia fursa hiyo ikiwa wanachangia GPE wanasaidia nchi zingine Barani Afrika na sisi pia Tanzania tunaweza tukapata fursa hiyo, lakini hata Benki ya Dunia hata IMF, AFDB zote zinajikita katika kutekeleza katika eneo hili pamoja na UNICEF. Kwa hiyo mimi naamini kwamba fursa hizi zipo, ikiwa tu tutaamua kulibeba jambo hili kwa uzito unaotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuhitimisha kwa kuiomba sana Serikali kwa kumuomba sana Profesa Adolf Mkenda, kwa sababu natambua anajua umuhimu wa chakula na lishe kwa Watoto, umuhimu wa chakula na lishe katika ufaulu. Tutafanya yote na yote yanaweza yakawa yasiwe na tija inayotakiwa au tija inayotarajiwa endapo tutaendelea kuruhusu watoto wetu asilimia 70 waendelee kuwa wanaenda shule na wanakaa na njaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa kuchangia katika hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje. Kwanza kabisa napenda kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa alizoweka za kubeba ajenda ya diplomasia ya uchumi na tayari tumeona matokeo chanya katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu nitajikita eneo hili la diplomasia ya uchumi. Tunaposema na diplomasia ya uchumi ina maeneo mengi na mimi kwa muktadha wa mchango huu nitagusia maeneo matano. Eneo la kwanza ni ziara za viongozi wetu wa Kitaifa kwenda nje ya nchi. Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziara hizi zimeleta mafanikio makubwa ambayo tumekuwa tukiyaona, jambo ambalo bado linahitaji litiliwe mkazo na liimarishwe ni namna gani Wizara ya Mambo ya Nje, itatupa taarifa ya utekelezaji wa yale mambo makubwa na mafanikio yanayotokana na ziara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni uwekezaji kutoka nje ya nchi. Kupitia diplomasia ya uchumi Tanzania imefunguka na tumekuwa tukiona wawekezaji wengi wakija Tanzania, lakini jambo ambalo bado linahitaji kutiliwa mkazo ni kituo chetu cha uwekezaji - TIC bado hakina mamlaka ya kutoa huduama ya one stop center, kwa muktadha huo wawekezaji wanakuwa wanakuja ndani ya nchi wakiwa na matarajio ya yale ambayo yalikubaliana katika aidha TIC au kupitia ziara za viongozi wetu, lakini wanapokuja hapa nchini kunakuwa na mkanganyiko baina ya yale yaliyokubaliwa pamoja na utekelezaji aidha ngazi ya Tawala za Mikoa au Serikali za Mitaa kwa maana ya Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hapa tunahitaji kuweka jitihada za maksudi kabisa ili kuhakikisha kwamba uwekezaji wa kutoka nje ya nchi wanapokuja hapa nchini mambo yawe mororo kusiwe kuna vikwazo au mkwamo wa aina mabalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ni biashara kati ya Tanzania na nchi zingine. Nawapongeza sana Wizara ya Mambo ya Nje, tumekuwa tukiona kila ziara za Wakuu wetu wa nchi sekta binafsi pia inakuwa inashiriki. Naomba nisisitize ushirikishwaji na ushiriki wa sekta binafsi hautakiwi kuwa tu pale ambapo kuna ziara za viongozi wetu wakuu, bali lazima tuweke jitihada za kuhakikisha kwamba sekta binafsi inatambua fika fursa zilizoko nje ya nchi na sekta binafsi kule nchi za nje na wenyewe wanatambua fursa zilizoko ndani ya Tanzania ili Wizara ya Mambo ya Nje iendelee kuwa kiungo baina ya sekta binafsi nchini Tanzania na sekta binafsi nchi za nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu Wizara hii ya Mambo ya Nje inaifungulia njia Tanzania duniani, lakini utekelezaji wa mambo mengi yanafanyika kwenye Wizara za kisekta, hapa ndipo iko changamoto bado hakuna mkakati thabiti wa namna gani ambavyo Wizara ya Mambo ya Nje itaendelea kusimamia utekelezaji wa fursa mbalimbali. Utekelezaji wa maazimio mbalimbali katika Wizara zingine za kisekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la nne ni misaada kwa ajili ya maendeleo ya jamii. Tumekuwa tukiona kupitia ziara za viongozi wetu, Wakuu wa Nchi, pia tumekuwa tukiona kupitia ziara za Wakuu wa Nchi zingine wanapokuja hapa Tanzania. Zinatolewa rasilimali fedha kwa maana ya misaada kwa ajili ya maendeleo ya jamii, lakini jambo ambalo bado linahitaji kutiliwa mkazo ni fedha zile za misaada bado utekelezaji wake zinakabidhiwa katika mashirika yasiyo ya kiserikali kwa maana NGO’s za nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Wizara hii inalo jukumu la kuona namna gani ambavyo wanaweza wakaisemea sekta ya NGOS za Tanzania, ili asilimia kubwa, zile rasilimali fedha zinazoingia Tanzania ziweze kutekelezwa na sekta ya NGOS za Tanzania. Kwa kufanya hivyo ndivyo ambavyo tutajihakikishia kwamba misaada inayoingia nchini inafanya kazi kwa kulinda na kwa kuzingatia misingi ya mila, desturi, tamaduni pamoja na yale ambayo yako kwenye Katiba yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili naamini kabisa halipaswi kuachiwa kwenye Wizara za kisekta kwa sababu, Wizara ya Mambo ya Nje ndiyo inaweza ikajadiliana na nchi nyingine kwa kutumia diplomasia ya uchumi kuona namna gani ambavyo fedha hizi za misaada zinapoingia nchini, basi NGOS za Tanzania ziweze kupata jukumu la kutekeleza ili kulinda; moja, ajira za Tanzania; na pili, fedha hizi ziendelee kuzunguka katika mnyororo wa thamani wa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tano ni suala la masomo na ajira za nje ya nchi. Tumesikia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri pamoja na hotuba ya Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu suala la diaspora. Tunapoongelea diaspora kuna Watanzania wenye uraia wa Tanzania, kuna Watanzania ambao wana asili ya Tanzania, lakini wana uraia wa nchi nyingine na kuna Watanzania ambao wako masomoni nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara, imezindua Diaspora Digital Hub tarehe 22 mwezi wa tano. Hii itatuwezesha kujua idadi halisi ya diaspora tulionao na wana taaluma zipi? Halikadhalika, liko jambo ambalo bado Wizara hii inahitaji kufanya. Nikiongelea kwa upande wa masomo, wapo vijana ambao wanapata fursa za masomo na wanapata fursa za scholarship kwa maana ya ufadhili wa masomo, lakini vijana hawa wanapoomba visa wanapata changamoto na wanajikuta wananyimwa visa. Sasa wanaponyimwa visa wakati wamekidhi vile vigezo vya msingi, kijana huyu anakuwa hana pa kwenda. Napendekeza Wizara hii ione namna gani ambavyo itasaidia vijana ambao wanakidhi vigezo vya msingi wasinyimwe fursa ya kupata masomo nje ya nchi pasipo sababu maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija pia kwenye ajira. Lazima kama Tanzania, maadamu tumeamua kuingia kwenye diplomasia ya uchumi, lazima tuangalie kada zipi ambazo sisi kama Tanzania tuna ujuzi nazo; na ni nchi zipi ambazo zinahitaji kada hizo; ili Wizara hii ya Mambo ya Nje iweze kujadiliana kupitia diplomasia ya kiuchumi, Tanzania itaweza kupata kada zipi katika nchi hizo? Kwa kufanya hivyo, tutaweza kupata diplomasia ya uchumi kwa maana ya kuwa na ajira ya Watanzania wengi zaidi ambao wanafanya nchi za nje, kwa mfano, kwenye kada ya Udaktari, Unesi, Ualimu, na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ina zaidi ya wananchi milioni 60. Kwa takwimu ambazo zilitajwa mapema mwaka huu hapa Bungeni, tunao diaspora 1,500,000 tu. Kwa nchi yenye wananchi milioni 60, bado hapa tunahitaji kuweka jitihada za nguvu zaidi ili kuhakikisha tunaongeza tija ya Watanzania ambao wako nje ya nchi, na ziko fursa nyingi katika ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kwenye ajira, nitilie mkazo umuhimu wa Wizara hii ya Mambo ya Nje ione namna gani ambavyo Watanzania watapata fursa za ajira katika mashirika ya kimataifa. Miaka ya nyuma tulikuwa tuna Watanzania wengi sana kwenye mashirika ya kimataifa, nami naamini kupitia jitihada za makusudi kabisa za Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, tutaweza kupata fursa hizi za ajira kwenye mashirika ya kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kumteua Mheshimiwa Balozi Liberata Mulamula kuwa mgombea wa nafasi ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola. Hii ni nafasi nyeti sana. Hivyo, naiomba sana Wizara ya Mambo ya Nje, kupitia balozi zake na machineries nyingine tuweke jitihada kubwa kuhakikisha tunapata fursa hizi za ajira. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja tu ya kuhitimisha. Naomba niishauri Wizara hii ianzishe kurugenzi ya fursa ili kurugenzi hii itoe fursa kwa Watanzania, Watanzania waweze kuelewa fursa pamoja na sekta binafsi. Wizara hii itoe elimu kwa Watanzania tuweze kuelewa diplomasia ya uchumi maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado suala hili halieleweki ndani ya Serikali, Taasisi za Serikali, katika Halmashauri zetu, sekta binafsi na hata na sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha. Suala hili la hadhi maalum, nawapongeza sana Serikali kwa hatua ambazo wamechukua, lakini naomba sana tulinde kwa wivu mkubwa suala la ushiriki kwenye masuala ya kisiasa pamoja na ajira kwenye vyombo vya ulinzi na usalama. Ajira hizi na ushiriki wa kisiasa lazima ulindwe na uwe ni kwa ajili tu ya Watanzania. Haiwezekani mtu mwenye uraia wa nchi nyingine apate fursa ya kushiriki kwenye shughuli za kisiasa au apate fursa ya kupata ajira kwenye vyombo vya ulinzi na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali na Wizara hii, tulinde maeneo haya mawili kwa wivu mkubwa. Masuala ya kushiriki katika siasa, masuala ya ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama, hizi zilindwe ni kwa ajili ya Watanzania na Watanzania pekee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii ya kuchangia kwenye Bajeti Kuu ya Serikali. Napenda kuanza kwa kuipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti Kuu ya Serikali napenda kuchangia katika maeneo manne ambayo yaligusiwa katika hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali. Eneo la kwanza ni matumizi ya TEHAMA na internet. Naipongeza Serikali kwa kutambua umuhimu wa matumizi ya TEHAMA na internet katika utekelezaji wa kazi zake na uamuzi huu utapelekea kuongeza chachu katika kufikisha huduma ya TEHAMA na internet katika maeneo yote nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tufanikishe hilo kwa uharaka, napenda kurejea ushauri niliotoa wakati nachangia kwenye bajeti ya Wizara inayosimamia masuala ya TEHAMA kwamba wakati umefika sasa Serikali itambue community networks kama njia mbadala ya kufikisha huduma ya internet kwenye maeneo ambayo bado hayajaunganishwa. Katika hili nina habari njema, wiki iliyopita katika Mkutano Mkuu wa Maendeleo ya Mawasiliano Duniani uliofanyika Kigali na nashukuru kwamba Mheshimiwa Waziri Nape Nnauye alikuwepo kwenye mkutano ule, Nchi zote Wanachama wamepitisha Azimio namba 37 ambalo limetambua community networks kama njia mbadala ya kufikisha haraka huduma ya TEHAMA na internet kwenye maeneo ambayo bado hayajaunganishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kusisitiza kwa Serikali, ili tutimize dhamira hii ya Serikali ya kutumia TEHAMA na teknolojia katika maeneo yote ikiwemo maeneo ya pembezoni, basi wakati umefika pia na Tanzania tutambue rasmi community networks kama njia mbadala.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la pili, napenda kuishukuru Serikali kwa kuamua kuanzisha dirisha maalum la kuhudumia watoto wanaotoka kwenye kaya maskini katika Mfuko wa Maendeleo wa TASAF. Hapa narejea wakati nachangia katika bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, nilipendekeza kwamba Serikali ione namna gani ya kutumia Mfuko huu wa TASAF kuwezesha watoto wa kike wanaotoka kwenye kaya maskini wapate msaada wa taulo za kike ili wasiendelee kukosa shule kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba wakati akihutubia, alisema kwamba dirisha hili jipya kwa ajili ya watoto wanaotoka kwenye kaya maskini litatumika kuwawezesha watoto wanaotoka kwenye kaya maskini kupata mahitaji maalum. Hivyo ningeomba kwa unyenyekevu mkubwa wakati Mheshimiwa Waziri anakuja kuhitimisha hoja yake atuainishie bayana haya mahitaji maalum ni yapi na naendelea kusisitiza katika hayo mahitaji maalum ni muhimu sana suala la msaada wa taulo za kike kwa watoto wa kike wanaotoka kwenye kaya maskini lijumuishe ili mtoto wa kike asiendelee kukosa shule kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la tatu, naishukuru sana Serikali kwa kupendekeza maboresho kwenye Sheria ya 148 ili kuwezesha Serikali kukusanya kodi za biashara za mtandao (online businesses) pamoja na digital services. Suala hili nilishauri hapa Bungeni mwaka jana na hii inadhihirisha kabisa kwamba kwa hakika Serikali ya Chama Cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ni Serikali iliyo sikivu na inaendelea kutupa moyo sisi Wabunge kuendelea kuishauri Serikali kwa ari na nguvu ili kuhakikisha kwamba tunachangia maendeleo endelevu ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili Serikali iweze kukusanya kodi ipasavyo, lazima pia tufanye maboresho kwenye Sheria ya VAT ili TRA waweze kutoza kodi makampuni ambayo yamesajiliwa nje ya nchi. Nitatoa mfano mdogo, DSTV wanatoa huduma hapa Tanzania, lakini hapa Nhini Tanzania kuna agent, pesa zote tunazolipa katika kuangalia DSTV zinalipwa Afrika Kusini na kanzidata ya wateja wa DSTV ipo Afrika Kusin. Kwa mantiki hiyo ni ngumu kwa Serikali yetu kupitia TRA kupata uhakika DSTV ina wateja wangapi hivyo kujua inatakiwa ilipwe VAT ya kiasi gani. Kwa hiyo pamoja na kwamba tunaenda kufanya maboresho ya hii Sheria 148 ni lazima Serikali ifanye haraka kuleta ile sheria ya data protection ili ndani ya ile sheria iwe ni lazima kwa kampuni hizi za kibiashara kutoa taarifa zao za wateja (sharing of debtor), kati ya hizi biashara na Serikali ili tuweze kupata uhakika maana zile data ni data za Watanzania iweje ziwe nje ya nchi na sisi ndani ya nchi tusiwe na access nazo. Kwa hiyo Sheria ya Data Protection ije ili tuweze kuhakikisha kwamba, kunakuwa hakuna mianya yoyote ya ukwepaji wa kodi katika biashara ambazo aidha zinafanywa online business ama zinatoa digital services au zinatoa huduma kwa kutumia satellite.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la nne, naipongeza sana Serikali kwa uamuzi wa kwamba kila mtu kuanzia umri wa miaka 18 apate usajili wa TIN, kwa sababu usajili huu wa TIN utawawezesha vijana wetu kujiajiri ikiwemo na kupata leseni za udereva. Hata hivyo, natambua pia moja ya lengo la kufanya hivi ni kuongeza wigo wa walipakodi kwa maana ya kwamba kuanzia vijana wa miaka 18 watakapofikisha kipato kile ambacho kinaweza kutozwa kodi, basi wataweza kulipia kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa kwa unyenyekevu kabisa na kwa kutambua kwamba tunayo changamoto ya ajira kwa vijana, naomba kupendekeza kwa Serikali itoe msamaha wa kodi kwa biashara mpya zitakazoanzishwa au biashara zitakazorasimishwa za vijana kati labda umri wa miaka 18 mpaka 30 ili vijana ambao wamemaliza shule wanahitimu vyuo vya kati, wanahitimu Vyuo Vikuu waweze kujiajiri. Jambo hili linawezekana, Serikali inaweza ikatoa msamaha wa kodi kwa vijana walau kwa miaka mitatu ili itoe hamasa kwa vijana hawa kuanzisha biashara zao na kurasimisha. Naamini jambo hili linawezekana kwa sababu ikiwa Serikali inatoa misamaha ya kodi kwa wawekezaji kwa nini ishindwe kutoa misamaha ya kodi kwa vijana wetu wa Kitanzania ambayo itakuwa ni chachu ya wao kujiajiri, lakini vivyo hivyo itakuwa ni njia ya kupelekea kuongeza wigo wa walipakodi hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuhitimisha, naomba kwa unyenyekevu mkubwa sana nirejee suala la umuhimu wa Serikali kuweka msamaha wa kodi ya VAT kwenye pump za maji zinazotumia nishati ya jua (solar water pumps). Wakati Serikali inaendelea kupeleka jitihada ya kufikisha maji vijijini, inaendelea kufanya jitihada ya kufikisha umeme vijijini, ni muhimu sana kwa Serikali kuweka mazingira ambayo yatarahisisha upatikanaji wa maji, hivyo kufanikisha dhamira ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kuwatua akinamama ndoo kichwani. Vivyo hivyo suala hili la solar water pump pia lina mchango mkubwa sana katika sekta ya kilimo kwa maana ya kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku ya tarehe 9 mwezi Juni mwaka huu 2022 katika ziara ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan mkoani Kagera katika mkutano wa kati yake na wananchi wa Bukoba mjini na Mkoa wa Kagera kwa ujumla niliwasilisha ombi kwake Mheshimiwa Rais la kuona namna gani ambavyo Serikali itaweka msamaha wa kodi kwenye hizi solar water pumps. Wakati anahutubia Mheshimiwa Rais alifanya rejea kwenye suala hili la VAT kwenye solar pumps. Mimi binafsi naamini kitendo cha Mheshimiwa Rais kufanya rejea kwenye suala la VAT kwenye solar pumps ni kiashiria tosha kwamba Serikali lazima iangalie jambo hili kwa jicho la kipekee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri Dkt Mwigulu Nchemba atakapokuja kuhitimisha hoja yake, lakini pia katika Muswada wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2022/2023, jambo hili la msamaha wa kodi kwenye solar pumps ni jambo ambalo linahitaji liwekewe uzito. Natarajia kwamba ni jambo ambalo litakuwemo na Serikali italichukua kwa uzito wake ili kuhakikisha kwamba tunawatua akinamama ndoo kichwani, lakini pia tunahamasisha kilimo cha umwagiliaji ambacho ndiyo sera ya Serikali hii ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye Taarifa yetu ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii. Napenda kuanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa anazozifanya za kuimarisha haki za wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi hizi zinaenda sambamba kabisa na namna ambavyo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Katiba na Sheria wameanzisha Samia Legal Aid Campaign ambayo inalenga kwenda kutatua maeneo mbalimbali ya changamoto za wanawake kupata haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika, namshukuru sana Mheshimiwa Spika na Wabunge wenzangu wote ambao tulichangia katika Miswada ya Sheria ambazo zinahusu masuala ya siasa na uchaguzi, na kwa namna ambavyo tuliibeba agenda ya wanawake na hadi kupelekea kuweza kuongeza vitendo vya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia kama moja ya kosa la uchaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo, mchango wangu utajielekeza katika maeneo manne yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ni Sheria ya Ukatili wa Kijinsia kwa maana ya GBV; tukirejea wakati tunajadili hapa Bungeni kwenye kupitisha Muswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, Mheshimiwa Waziri Jenista Mhagama alielezea namna ambavyo Serikali imetambua ukubwa wa tatizo la ukatili wa kijinsia na kwamba sasa Serikali iko mbioni kuleta Bungeni Muswada wa Sheria ya Ukatili wa Kijinsia kwa maana ya GBV.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nijielekeze katika eneo hili. Serikali ifanye jitihada ya haraka ituletee huu Muswada Bungeni kwa maana ya Muswada wa Sheria ya GBV na Sheria hii itakayokuja hapa Bungeni isijielekeze tu katika kuweka makosa na adhabu zake yaani offences na penalties, lakini pia ijielekeze katika kutoa elimu ya namna ya kupambana na kuthibiti vitendo vya GBV na vilevile ijielekeze katika namna ya kutoa compensation kwa wale wahanga ikiwemo na adhabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo napenda kusisitiza kwamba Sheria hii ya GBV isiyajumuishe makosa yote kwenye kundi moja, badala yake iainishe makosa kwenye makundi tofauti kulingana na jinsi yalivyo. Kwa mfano, ukatili wa kijinsia mitandaoni, kwenye ndoa, nyumbani, watoto na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni kuhusiana na umiliki wa ardhi kwa wanawake. Kumekuwa na changamoto kubwa sana ya umiliki wa ardhi kwa wanawake japokuwa Sheria ya Ardhi ya Mwaka 1995 inazingatia kwamba umiliki wa ardhi kwa wanawake na inaainisha iwe vipi, lakini kuna Sheria mbalimbali ambazo zinakinzana na jambo hili. Kwa hiyo, hapa napenda kupendekeza kwa Serikali kwamba lazima ije na mfumo wa kisheria na kikanuni ambao utaweza kurahisisha namna ya kuhakikisha wanawake wanamiliki ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kipekee nampongeza Mheshimiwa Jerry Silaa, Waziri wa Ardhi pamoja na Mama yangu Mheshimiwa Waziri Dkt. Dorothy Gwajima kwa namna ambavyo wanashirikiana kwa ukaribu kutatua changamoto za umiliki wa ardhi kwa wanawake likiwemo eneo la mirathi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili halipaswi kuwa kwa utashi wa viongozi, kwa hiyo, ni vyema sasa Serikali ione namna ambavyo itaweka mfumo rafiki kuhakikisha masuala ya wanawake ya umiliki wa ardhi yanaratibiwa ipasavyo. Kwa mfano, kunaweza kukawa na dawati la umiliki ardhi kwa wanawake na watoto wa kike ndani ya Wizara hii inayosimamia masuala ya Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, halikadhalika hivyo hivyo kwenye Wizara ya Ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ni kuhusu MTAKUWA. Wote tunafahamu kwamba Serikali iko mbioni kukamilisha Mpango wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto Awamu ya Pili. Sasa katika maeneo haya, yako maeneo mawili ambayo napenda kusisitiza kwa Mheshimiwa Waziri Dkt. Dorothy Gwajima kuhakikisha kwamba MTAKUWA unayazingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari hapa Bungeni tumeshatambua kisheria kwamba vitendo vya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia katika uchaguzi ni kosa la uchaguzi. Vivyo hivyo basi na kwenye MTAKUWA itakuwa ni vyema pia kutambua unyanyasaji na ukatili wa kijinsia katika uchaguzi kama moja ya maeneo ambayo MTAKUWA lazima iangazie. Jambo la pili, ni ukatili wa kijinsia mtandaoni kwa wanawake, mabinti, watoto na jinsia zote. Ni muhimu sana jambo hili nalo likazingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la nne ni unyanyasaji katika maeneo ya kazi. Tanzania imeridhia mikataba mbalimbali ya kidunia pamoja na ya kikanda. Mathalan, kwa haraka haraka Tanzania imeridhia Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Binadamu, Article 2 na 21 ambayo inaangalia haki za kisiasa bila ubaguzi, pia imeridhia Mkataba wa Haki za Kisiasa kwa Wanawake wa1952, pia imeridhia Beijing Declaration and Platform for Action ya Mwaka 1995; pia tumeridhia Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu Juu ya Haki za Wanawake ambayo hii ni Itifaki ya Maputo 2003; vilevile tumeridhia Itifaki ya SADC ya Usawa wa Kijinsia 2008 pamoja na Mkataba wa Kuondoa Aina Zote za Ubaguzi Dhidi ya Wanawake (CEDAW) 1979, lakini Tanzania tuliridhia 1985.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia upo Mkataba mmoja wa Kimataifa ambao bado Tanzania hatujaridhia. Tanzania bado hatujaridhia Mkataba wa C190 ambayo inahusu sexual harassments at work. Yaani kwa maana kwamba bado hatujaridhia Mkataba wa Kimataifa…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.


TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Neema, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jacqueline Msongozi.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Neema Lugangira kwa namna ambavyo anachangia hasa kwenye hili eneo la ukatili wa kijinsia makazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka tu niongezee kwake kwa maana ya taarifa, kwamba siyo tu makazini kwa maana ya maofisini kama alivyosema, lakini pia kumekuwa na ukatili wa kijinsia kwenye maeneo ya kazi ambayo kwa wafanyakazi wa majumbani. Kwa lugha nyingine ni ma-house girl na ma-house boy. Kumekuwa na ukatili mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, anapozungumza, basi aongeze na hilo ili sasa Muswada utakapokuwa unaletwa hapa Bungeni, basi uzingatie pia kwenye maeneo haya kwa sababu kwenye maeneo haya ni waathirika wakubwa pia, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Neema, taarifa unaipokea?

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hiyo taarifa na huko ndiko ambako nilikuwa naelekea, kwa sababu tunapoongelea huu Mkataba wa Kimataifa wa C190 wa Sexual Harassment, maeneo ya kazi ni maeneo yote yakiwemo majumbani. Pia uko Mkataba wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) ambao una vipengele mbalimbali. Katika itifaki hizi za mikataba ya kimataifa na kikanda, siyo lazima nchi iridhie vipengele vyote. Kwa hiyo, sisi kama Tanzania tunaweza tukachambua tukachagua maeneo ambayo yanaweza yakaendana na tamaduni, desturi na namna ambavyo Tanzania tunaendesha masuala yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea ukatili huu wa kijinsia na unyanyasaji kwenye maeneo ya kazi ni pamoja…
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Neema, taarifa kutoka kwa Naibu Waziri Mheshimiwa Patrobass.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Nampongeza sana Mheshimiwa Neema, ana ujuzi na ubobevu mzuri kwenye hayo maeneo, lakini ni muhimu wakati anachangia mchango wake mzuri akumbuke pia tayari kwa Tanzania tumeshazingatia maeneo mengi. Tunayo Sheria yetu ya penal code ambayo ilifanyiwa maboresho baada ya kuwa na Sexual Offences Special Provincial Act ya Mwaka 1998.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria hii ilikuwa inahusiana na masuala ya makosa yote yanayofanana na masuala yanayohusiana na unyanyasaji wa kijinsia. Utakumbuka kuna kipindi ilikuwa hata kukonyeza ni kosa, kwa hiyo, ikawekwa kwenye Sheria yetu ya Penal Code. Sheria Penal code iko extensive sana kwa maana kwanza ina-establish offence na pili inaeleza adhabu na utendekaji wa kosa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ili aweze kuendelea na mchango wake, kwenye Sheria yetu ya Rushwa na Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, zimetambua makosa hayo specific, masuala ya sexual harassments kuwa ni makosa. Kwa hiyo, hatuko nyuma, tusiseme kama vile Tanzania iko nyuma sana.

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Neema malizia mchango wako, muda umeisha.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba unilinde, nataka tu kumsahihisha kidogo kaka yangu Wakili mbobezi kabisa, hakuna ambapo nilisema kwamba Tanzania haijafanya vizuri, na ndiyo maana nilianza kwa kutambua mikataba yote ambayo Tanzania imeridhia Kimataifa na Kikanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nikasisitiza na nikatambua kauli ya Serikali wakati tunajadiliana hapa kwenye Miswada ya Sheria za Uchaguzi na masuala ya siasa kwamba Serikali yenyewe imetambua kwamba kwa ukubwa wa changamoto ya masuala ya ukatili wa kijinsia, ije na sheria mahususi ya GBV. Hata mwaka 2022, SADC tayari wametoa SADC GBV Model Law. Kwa hiyo, ni kwa muktadha huo huo najaribu kuainisha kwamba, ni lazima sasa ile ahadi ya Serikali iliyoitoa ndani ya Bunge hili siku ya Ijumaa wiki iliyopita, sheria ile ije kwa haraka ili maeneo haya yote ya GBV kwa umahususi wake yaweze kuzingatiwa badala ya ilivyo hivi sasa. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Neema.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika Wizara hii. Naomba nianze kwa kusema naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, Sera yetu ya Kilimo hapa nchini inasema kwamba Mgani Mmoja, Kijiji Kimoja. Kama tunavyofahamu, tuna vijiji takribani 12,000 lakini hadi sasa tuna wagani 7,000; kwa hiyo, tuna upungufu wa wagani kama 5,000.

Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa napenda kuipongeza Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, hususan Mheshimiwa Waziri, Prof. Adolf Mkenda, pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Hussein Bashe, kwa jitihada kubwa walizoweka kuleta mageuzi kwenye huduma ya ugani, ikiwemo kutenga bajeti kwa ajili ya kuwanunulia hawa Maafisa Ugani vitendeakazi kama pikipiki. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna changamoto ambayo naiona. Hii changamoto ni kwamba tunategemea Afisa Ugani huyu awe mtaalam wa kila kitu; ajue mazao yote, ajue masuala ya mbolea, masuala ya wadudu, masuala ya madawa, fungus, ukungu na kadhalika. Jambo ambalo siyo rahisi.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka miaka ya nyuma Serikali ilishaliona hili na ilianzisha kitu kinachoitwa Ward Agriculture Resources Centers, yaani Vituo vya Rasilimali ya Kilimo ngazi ya Kata. Kama sikosei vituo hivi vilianzishwa kwenye kata 200 hapa nchini. Pamoja na kuanzisha vituo hivi Serikali iliweka watalaam kwenye vituo hivi na iliweka vitendea kazi kama kompyuta, generator, screen za kufundishia na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza sana Wizara kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, wamesema wanaenda kuvifufua hivi vituo, lakini ningependa kushauri kwamba, ni lazima Wizara iangalie hivi vituo kweli vifanye kazi ambayo ilikusudiwa. Nasema hivi kwa sababu hivi sasa, kwa kuwa hivi vituo vipo chini ya halmashauri, kwenye halmashauri nyingi vituo hivi havifanyi kazi iliyokusudiwa ya kuendeleza kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano pale Chamwino, kituo hiki badala ya kufanya kazi ya kuendeleza kilimo kinatumika na TARURA. Kwa hiyo ningependa kuishauri Serikali ipitie upya vituo hivi na ione kama vinatumika kadri ambavyo inafaa na kama kuna changamoto basi vituo hivi virudishwe viwe chini ya Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapo hapo kwa miaka mingi sasa halmashauri zimekuwa hazitengi bajeti ya huduma ya ugani, ambapo hii ni changamoto kubwa na hatuwezi kuendeleza kilimo wakati ni hizi halmashauri karibu asilimia 70 ya mapato yao ya ndani yanatokana na kilimo, lakini utengaji bajeti wa huduma ya ugani hawatengi. Kwa hiyo hili nalo ningependa katika kuhitimisha najua linahusu zaidi Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Mheshimiwa Waziri yupo hapa pengine atatuambia anapanga vipi kuhakikisha kwamba hizi halmashauri zinatenga bajeti ya huduma ya ugani. Naamini kwamba lengo zima la kuanzisha vituo hivi lilikuwa ni kuhakikisha tunaimarisha huduma ya ugani. Tukifanya hivyo tutaweza kuongeza tija na muhimu zaidi kuongeza pato la mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo langu la pili ambalo ningependa kuchangia ni pato la mkulima. Kwa muda mrefu sana tumekuwa tukiongelea bei ya mkulima na kabla sijaingia hapa Bungeni nilikuwa nafanya kazi kwenye Shirika ambalo lipo chini ya Wizara ya Kilimo SAGCOT yaani Southern Agriculture Growth Corridor of Tanzania kama Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Wezeshi kwenye Biashara, nimefurahi nimemwona bosi wangu Mr. Geofrey Kilenga yupo ndani ya ukumbi huu wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kipindi kirefu tunaongelea bei ya mkulima, lakini nadhani wakati umefika sasa tuongelee pato la mkulima, kwa sababu tunapoongelea pato la mkulima lina variable mbili. Variable moja ni price, variable ya pili ni quantity and quality. Sasa tumekuwa tukiweka jitihada kubwa sana kwenye bei, tunasahau hii variable ya pili ambayo ni muhimu ya quantity and quality.

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu wengi wameongelea tija yetu ya kwenye kilimo, nitatoa mfano mdogo, wenzetu wa Zambia kilo moja ya mahindi wanauza Sh.250 mpaka Sh.300 ya Tanzania na wenyewe wakiuza kwa bei hiyo wanarudisha gharama zao zote yaani wana-break even, lakini kwetu sisi Tanzania ili kufikia hiyo break even point lazima kilo moja ya mahindi tuuze Sh.500.

Mheshimiwa Spika, vivyo hivyo ipo hata kwenye pamba, nchi ambazo tunashindana nazo India, Brazil, China, Egypt, wao wanazalisha kwa eka moja kilo 1,000 mpaka kilo 1,250. Kwa hiyo wao wakiingia sokoni wanaweza wakauza kwa bei ya Sh.500 na waka-break even, lakini sisi kwa sababu tija yetu ni ndogo tunazalisha wastani wa heka hiyo hiyo moja kilo 250 hatuwezi kuuza kwa ile bei ya Sh.500 mpaka ifike angalau bei ya Sh.1,000.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hilo, ndiyo maana napendekeza kwamba ifike mahali Wizara ya Kilimo ianze kuongelea pato la mkulima na siyo bei ya mkulima. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kuongeza tija ambayo itaongeza mchango katika pato la Taifa kwa sababu tunasema kila siku asilimia 65 ya Watanzania wapo kwenye kilimo, lakini bado tunachangia asilimia 27 tu kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo inatokana na kwamba tija yetu bado ni ndogo na hiyo inatokana kwamba kila siku wimbo wa Wizara ya Kilimo ni kwamba bei ya mkulima. Kwa hiyo naomba kusisitiza tutoke kwenye bei ya mkulima twende kwenye pato la mkulima. Na na… (Makofi)

SPIKA: Bei ya mkulima ndiyo nini?

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, bei ya mkulima ni ile ambayo inakuwa inapangwa, yaani unakuta mkulima akishakuwa amepata mavuno, Wizara ya Kilimo inaitisha wadau, wanakaa halafu wanapanga bei ya mkulima. Kama wanaweza wakaitisha wakulima wazao wa pamba wanakaa wanapanga kwamba bei ya kilo moja ni Sh.1000 au wanaenda kwenye mnada. Sasa ninachojaribu kusema kwa kufanya hivyo hatukuzi tija inakuwa kama vile tunafidia ule upungufu wa tija ambao tulionao. Tukijikita katika pato la mkulima ina maana zile variable zote mbili, bei maana ya price, quantity na quality tutakuwa tumezifikia

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa hii na naunga mkono tena hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii. Kwanza kabisa ningependa kwa kuanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa ziara yake ya kwanza aliyofanya nchini Kenya ambayo imeleta matokeo makubwa sana katika economic diplomacy ambayo tunaihitaji na kama tutakuwa tunafuatilia weekend hii Serikali ya Tanzania na Kenya wamekubaliana kuondoa tozo za biashara 30 na pia kuna mchakato wa kuondoa tozo 34. Kwa hiyo, hii ni matokeo ya jitihada kubwa za Mheshimiwa Rais na hapa pia nimpongeze Waziri wa Viwanda na Biashara kwa kufanikisha jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile ningependa kusisitiza kwamba, mtazamo wa Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kuhusu Kenya kwamba, Kenya sio adui yetu uungwe mkono, Kenya ni mshindani mwenzetu, Kenya wanatupa changamoto. Hivyo tusiwaogope, tunawaweza na tunaweza kuwakabili na ninasema hivi kwa sababu hata nchini Tanzania tupo Watanzania wengi ambao tumesoma nchini Kenya, kwa hiyo, tunawafahamu na tunaweza kushindana nao ipasavyo tusiwaogope. (Makofi)

Aidha, napenda niungane na Wabunge wenzangu ambao wametoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuhusiana na kutengeneza safu mpya kwenye Wizara ya Mambo ya Nje iliyojaa wabobezi kwenye fani hii ya diplomasia chini ya uongozi makini wa Balozi Mwanamama Liberata Mulamula, Naibu Waziri Balozi Mbarouk, Katibu Mkuu Balozi Sokoine, Naibu Katibu Mkuu Balozi Fatma Rajabu lakini pia na Chief of Protocol Balozi Mndolwa ambao kwa ujumla wao wote tuna imani nao kubwa sana na sasa tunaendelea kuona diplomasia ya nchi yetu ikipaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ningependa kugusia suala la diaspora; hili jambo lilishajadiliwa sana na tulishapiga hatua ambapo diaspora hawa mikutano mbalimbali ilifanyika nje ya nchi kukusanya maoni ya diaspora lakini hata na diaspora walishirikishwa katika kutoa maoni kwenye Katiba mpya ambayo inapendekezwa. Sasa nimefurahi katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amegusia suala la diaspora lakini na hata katika mapendekezo ya Kamati nao pia wamegusia suala la diaspora.

Mheshimiwa Spika, kati ya mwaka 2010 hadi 2015 zilifanyika ziara nyingi sana nje ya nchi kama ambavyo nimesema kukusanya maoni na hawa diaspora pia walishiriki kwenye huu mchakato wa Katiba mpya na yote haya yalipelekea kuanzishwa kwa Idara ya Diaspora ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje ambapo kulikuwa na Mkurugenzi mwenye jukumu la kufanya co-ordination na ufuatiliaji. Hivi sasa jambo hili ni kama tumerudi nyuma kwenye hii ajenda nzima ya diaspora, kwa sababu hivi sasa kuna sheria ambazo zinamzuia Mtanzania anayeishi nje kumiliki ardhi, lakini zipo pia sheria ambazo zinamnyima Mtanzania anayeishi nje ya nchi haki ya msingi kwa mfano hata kurithi mali za wazazi wake, Mtanzania anayeishi nje ya nchi hawezi kurithi mali ya baba yake au mama yake kwa sababu sheria zimeweka hicho kizuizi.

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo mimi ambacho ningependa kupendekeza ni kwamba Waziri au Wizara ya Mambo ya Nje ije na sera ya diaspora kwa sababu kama tunavyofahamu nchi za wenzetu wanatumia diaspora katika kuendeleza na kukuza uchumi pamoja na uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, ninaendelea kusisistiza kwamba Serikali itunge sera ya diaspora na sera hii ni muhimu kwa sababu jambo hili haliwezi kuendeshwa na Wizara ya Mambo ya Nje peke yake, suala hili linahusu Uhamiaji, linahusu Ardhi na mambo kadha wa kadha.

Mheshimiwa Spika, Mbunge mwenzangu aliyetoka kuzungumza ametolea mfano wa India, lakini ningependa kufafanua kidogo India walichofanya wamewapa watu wa India wanaoishi nchi za nje kitu kinachoitwa Peoples of India Origin (PIO) na hii PIO inamruhusu yule mwenye passport ya PIO kuingia India na kutoka muda wowote bila visa, inamruhusu kuwekeza kwenye hiyo nchi, inamruhusu kufanya kazi kwenye sekta zote kasoro sekta ya ulinzi na usalama na jambo lingine ambalo hawaruhusiwi kufanya ni kujishughulisha na masuala ya kisiasa na kupiga kura. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa mantiki hiyo, na mimi ningependa kupendekeza na sisi kama Tanzania tufike huko, hatuwezi kwenda huko bila kuwa na sera ya diaspora na sheria ambayo itatuelekeza ni namna gani tutatoa fursa kwa hawa diaspora, na tusichanganye mambo mawili diaspora na uraia pacha, hili la uraia pacha tumeshalijadili na limeonekana lina ugumu, hivyo lisituchukulie muda, lakini hili la diaspora ninaamini lipo ndani ya uwezo wetu na hata sasa hivi diaspora wananunua viwanja, wanawekeza lakini wanafanya hivyo kwa kutumia njia ambazo sio rasmi kwa kutumia ndugu, jamaa na marafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunachotakiwa tufanye ni tuwe tu na sera ya kuweka hili suala rasmi na kupitia hiyo tutaweza kujua tuna diaspora wangapi tutaweza kujua mchango wa diaspora kwenye ukuaji wa uchumi wetu. (Makofi)

Kwa hiyo, kwa kumalizia ningeomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atuambie na atupe commitment ya Serikali ya kuja na sera ya diaspora ambayo itawezesha Watanzania wanaoishi nje kuchangia kwenye maendeleo ya nchi yetu na kutupa rasilimali fedha ambayo tunaihitaji kwenye uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii na nianze kusema naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, vilevile napenda kusema kwamba ajira yangu ya kwanza ilikuwa kwenye sekta hii ya nishati na madini. Kipekee kabisa napenda kumshukuru yeye mwenyewe Waziri Kalemani, Mheshimiwa George Simbachawene, Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo pamoja pia na Mheshimiwa Jenista Muhagama kwa ulezi bora walionipa hadi kufikia hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia eneo la usambazaji wa gesi nchini. Wengi tunafahamu kwamba TPDC haitekelezi zoezi la usambazaji wa gesi nchini kwa kasi inayotakiwa vilevile nchini Kenya na Uganda wanahitaji kununua gesi kutoka kwetu. Napenda kugusia Sheria ya Oil and Gas Revenue Management ya 2015 ambayo Bunge lako Tukufu liliipitisha.

Mheshimiwa Spika, kwenye sheria hii ilikuwa imesema kwamba kutakuwa kuna mfuko maalum ambapo fedha zile zitatumika kuendeleza sekta ya mafuta na gesi nchini. Hivi sasa tunapoongea kutokea 2015 mpaka sasa mfuko huu una takriban shilingi za kitanzania bilioni 400 ambazo zimekaa tu kwa sababu kwenye sheria kiliwekwa kifungu kwamba fedha ile haiwezi kutumika mpaka mfuko ufikie asilimia 3 ya GDP.

Mheshimiwa Spika, itatuchukua muda mrefu sana kwa mfuko ule kufikia hiyo asilimia 3 na ndicho kiwango cha zaidi ya asilimia 3 ndipo ambapo TPDC itaruhusiwa kutumia kwa ajili ya kuwekeza kwenye mafuta na gesi asilia. Kwa hiyo, kwa unyenyekevu mkubwa sana napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri ailete ile sheria hapa Bungeni ifanyiwe maboresho ili sehemu ya ile shilingi bilioni 400 ambayo sasa hivi imekaa TPDC waweze kuitumia ili waweze kuendeleza miundombinu ya gesi, usambazaji wa gesi lakini pia kuuza gesi hii nchini Kenya na Uganda jambo ambalo litaendelea kutupa rasilimali fedha ambayo tunahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wengi tunaendelea kulalamika kwamba TPDC ipewe fedha lakini tofauti na REA mfano Wizara inatoa kiwango cha fedha kwenye REA lakini TPDC haipewi fungu lolote kwenye hili eneo la uendelezaji wa hii miundombinu kwenye sekta ya gesi asilia. Kwa upande mwingine tunayo shilingi bilioni 400 ambayo imefungwa kutokana na kile kifungu cha sheria. Kwa hiyo, naomba sana kwa unyenyekevu Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atuambie ni lini ataweza kutuletea maboresho ya ile sheria ili sisi kwa umoja wetu tuweke vifungu na maelekezo ya namna gani ambavyo TPDC itaweza kutumia sehemu ya fedha iliyopo ili isiendelee kukaa huku na sisi tunaendelea kupoteza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia, naomba niongelee Mkoa wangu wa Kagera. Sisi Mkoa wa Kagera toka Uhuru mpaka leo hatujawahi kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa tunategemea umeme wa Uganda na uhitaji wa umeme Uganda nao umezidi kukua kiasi kwamba hata na wao wananunua umeme kutoka kwetu. Kwa hiyo, napenda kupata kauli ya Mheshimiwa Waziri ni lini sisi Mkoa wa Kagera tutaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kwa sababu hali ilivyo sasa kuendelea kutuweka gizani; moja ni hatari kwa sababu sisi ni mkoa wa mpakani, lakini pili unaendelea kudhoofisha ukuaji wa uchumi wa Mkoa wetu wa Kagera. Kwa kuzingatia kwamba sisi ni mkoa wa mpakani na ni hatari kuendelea kutuweka gizani, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atupe uhakika ni lini atatuletea Gridi ya Taifa mkoani Kagera tukizingatia imeshafika mpaka jirani yetu Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana naunga tena mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii, nami ningependa kuchangia kidogo katika eneo hili la sheria ndogo. Kwa uwelewa wangu sheria ndogo zinapaswa zifuate utunzi wa sheria na kuhakikisha kwamba hazikinzani na yale ambayo yameelekezwa kwenye Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, na kati ya vitu ambavyo Katiba yetu inatambua ni pamoja na suala nzima la freedom of association na huu ndiyo msingi wa sekta ya Asasi za Kiraia kwa maana ya CSOs, NGOs na kadhalika ambao wanakuja pamoja kwa lengo la kuchangia maendeleo katika jamii.

Mheshimiwa Spika, sasa katika upande huu wa sheria ndogo ziko sheria ndogo ambazo zinatungwa na Halmashauri, lakini pia zipo kanuni ambazo zinatungwa na Mawaziri wenye dhamana ya maeneo husika. Hapa ningependa kurejea kwenye Sheria ya NGOs. Katika sheria hii ilitoa mwanya wa Waziri mwenye dhamana kuandaa kanuni kutunga kanuni na kati ya kanuni ambazo zimetungwa chini ya sheria hii ya NGOs ipo kanuni ambayo inataka NGOs kwa maana ya sekta Nzima ya Asasi za Kiraia pale ambapo zinapata ufadhili wa mradi wowote hata kwa kiwango cha milioni 20 uwasilishe lile andiko lake, uwasilishe pia na mkataba na nini ambacho unataka kwenda kufanya, uwasilishe kwenye ofisi mbili tofauti yaani unatakiwa uwasilishe kwenye Ofisi ya Msajili wa NGOs lakini pia Hazina na baada ya kuwasilisha hivyo vitu vyote huyu NGOs hawezi kutekeleza ule mradi mpaka apate kibali kutoka kwa msajili wa NGOs na Hazina, jambo ambalo kwa kawaida linaongeza mlolongo mrefu. (Makofi)

Kwa hiyo unakuta labda NGOs imegundua kuna changamoto fulani kwenye jamii, imetafuta ufadhili imepata ufadhili labda milioni 20/30 lakini hawezi kutekeleza mpaka apewe kibali na unakuta ufadhili ule kapewa labda mradi unatakiwa utekelezwe ndani ya miezi sita mpaka mwaka, mlolongo mzima huu wa mpaka kupata kibali unachukua miezi sita, kwa hiyo mpaka unakuja kupata kibali ile fedha inabidi umrudishie mfadhili au inakuwa ni muda mfupi sana umebaki kiasi kwamba huwezi kutekeleza ule mradi jinsi ambavyo umetakikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa jambo hili linafifisha ile financial freedom ya hii sekta ya Asasi za Kiraia, lakini mbaya zaidi unapelekea pia kuwapa changamoto wadau wa maendeleo kwa maana ya wafadhili wanakuwa na hofu kuona je, mradi utatekelezeka ndani ya muda ambao umepangwa?

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kukiri kanuni hii iliwekwa kwa nia njema kabisa ya kuhakikisha kwamba tunaimarisha uwazi na uwajibikaji kwenye Sekta ya Asasi za Kiraia, lakini hapo hapo tutambue ya kwamba hizi NGOs zote zinakuwa zimesajiliwa kwa hiyo Serikali kupitia Msajili wa NGOs imepitia katiba zake, imepitia malengo ikawapa usajili, kila mwisho wa mwaka wanatakiwa wawasilishe ripoti yao ya mwaka ya kazi/audited accounts.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi napenda kupendekeza hii kanuni Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana aiangalie upya ili pia basi hizi NGOs, sekta ya AZAKI kwa maana ya NGOs, CSOs, wanatakiwa watakapokuwa wanawakilisha taarifa zao za mwaka (audited accounts) pia wawasilishe mikataba ya zile fedha walizopata na namna walivyozitumia. Kwa sababu kinyume na hapo tunaenda kinyume na lengo zima ambalo kwanza limewekwa kwenye Katiba, lakini hata lengo la ile sheria mama ya NGOs ambayo inataka kuhakikisha ya kwamba Sekta hii ya AZAKI inachangia katika maendeleo ya jamii na sekta hii inafanya kazi kubwa sana kwa kushirikiana na Serikali na hata juhudi zake zimetambuliwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa hiyo kwa kumalizia napenda kuiomba sana Serikali kupita wizara husika izipitie upya kanuni hizi, lakini…

MHE: SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ninaomba nimpe taarifa anayezungumza kwa sababu mimi pamoja na wengine najua wamo hapa tumefanya kwenye NGOs kwa muda mrefu. Ni lazima upeleke taarifa kwenye Wizara husika na audited account huwa wanafanya hivyo kwa watu wa NGOs sijajua labda anazungumzia eneo lipi?

SPIKA: Nakuongezea dakika Mheshimiwa fafanua.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru kama alinisikiliza vizuri kwenye mchango wangu nilisema kwamba kila mwaka NGOs zinawasilisha taarifa zao za mwaka za hesabu, lakini pia zinawasilisha audited accounts, lakini kwenye kanuni imesema kwamba NGOs itakapopata mradi wa kuanzia shilingi milioni 20 isitekeleze mradi huo mpaka ipate kibali kutoka kwa Msajili wa NGOs na Hazina. (Makofi)

Kwa hiyo, mimi ninachoongelea hapa kwa sababu tunaongelea sheria ndogo na mojawapo ya sheria ndogo zipo za upande wa halmashauri, lakini pia zipo zile ambazo zinatungwa na Mawaziri wenye dhamana kupitia kanuni, kwa hiyo, hicho ndiyo nilichokuwa nakiongelea na ningependa na yeye ajielimishe zaidi katika eneo hili ili kwa pamoja tuweze kuishauri Serikali vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kurejea tena naiomba sana Wizara yenye dhamana ya masuala ya maendeleo ya jamii ipitie upya kanuni hizi ili iweze kuimarisha financial freedom ya sekta hii ya AZAKI maana hivi sasa inakinzana na inafifisha juhudi za sekta za AZAKI kuchangia katika maendeleo ya jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia napenda kumshukuru sana Waziri mwenye dhamana ya masuala ya maendeleo ya jamii kwa sababu mchango wangu kwenye bajeti ya Wizara hii niliiomba sana itusaidie ili ufanyike uchaguzi wa Baraza la NGOs la Taifa (NACONGO) ambalo liko ngazi ya Wilaya, Mikoa mpaka Taifa na hivi sasa uchaguzi huo unaendelea, kwa hiyo, napenda kumshukuru sana kwa kutusaidia katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, majuzi kwenye kikao chake na Baraza la Maaskofi wa Kikatoliki Tanzania alikumbushia kwamba yeye ni mwanaharakati na ni mwana-AZAKI pale ambako walipokuwa wanamtambulisha Askofu Kilaini. Kwa hiyo, na kwa kutumia hiyo hiyo napenda kuendelea kumwakikishia kwamba sekta ya Asasi za Kiraia tunamtambua kama mwana-AZAKI mwezetu na tunaahidi kuendelea kumpa ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza azma yake ya maendeleo ya jamii kwa Taifa letu na hakika tutafika pale ambapo anataka tufike kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa fursa hii na nakubaliana na maoni ya kamati husika, ahsante. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye hili Azimio la kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Afya ya Wanyama na Usalama wa Chakula na mchango wangu utajikita kwenye eneo zima la usalama wa chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kuishauri Serikali kwenye eneo zima la usalama wa chakula kwa maana ya inasimamiwa chini ya wapi? Good practice ni kwamba masuala ya usalama wa chakula yanapaswa kuratibiwa chini ya Wizara ya Afya kwa sababu kimsingi maana ya usalama wa chakula ni kuona namna gani ambavyo utalinda walaji wasipate changamoto zozote zinazotokana na madhara ya chakula. Jambo hili ni jukumu la Wizara ya Afya, lakini sasa hapa kwetu tulichofanya
tumeweka jukumu la usalama wa chakula kwa maana ya food safety chini ya TBS.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kuishauri Serikali, maadam tumeamua kuridhia azimio hili, basi lazima tukatafakari upya na tufanye mabadiliko ambayo yatawezesha suala la usalama wa chakula yawe chini ya Wizara ya Afya na siyo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo naipongeza sana Wizara ya Kilimo kwa sababu wameimarisha usimamizi kwenye afya ya mimea chini ya TPRI, lakini hivi sasa TBS ina majukumu mengi na haiwezekani aendelee kuwa na majukumu yale yale. Kwa hiyo, naendelea kusisitiza suala hili liwekwe chini ya Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile moja ya matakwa ya itifaki hii duniani chini ya Well Trade Organization, ni lazima nchi iwe ina Sheria ya Usalama wa Chakula. Tanzania bado hatuna Sheria ya Usalama wa Chakula. Kwa hiyo, napenda kusisitiza kwa Serikali, maadam tumeamua kuridhia azimio hili, basi Serikali ifanye jitihada ya haraka kutuletea Sheria ya Usalama wa Chakula ili tuendane na takwa hili la kidunia. Ndani ya nchi zetu za Afrika Mashariki, ni Kenya peke yake ambayo tayari wanayo Sheria ya Usalama wa Chakula. Kwa hiyo, kwa mantiki hiyo, sisi kuendelea kutokuwa na Sheria ya Usalama wa chakula, ina maana yako maeneo ambayo hatutaweza kunufaika ipasavyo. Kwa hiyo, nasisitiza Serikali ije na Sheria ya Usalama wa Chakula kwa maana ya Food Safety na siyo Food Security. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nishauri kuhusu suala la usimamizi wa usalama wa afya ya mazao ya kilimo. Usimamizi wa afya ya mazao ya kilimo inapaswa iwe chini ya Wizara ya Kilimo na siyo TBS. Kwa hiyo, naomba niishauri Serikali kupitia Wizara ya Kilimo ione ni namna gani baada ya azimio hili litakapokuwa limeridhiwa na Bunge lako Tukufu, basi usimamizi wa masuala yote ya usalama wa afya ya mazao ya kilimo yawe chini ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia mara baada ya sisi kuidhinisha na kuridhia azimio hili, ni muhimu sana Serikali kupitia Wizara ya Kilimo iweke jitihada kubwa ya kutoa elimu kwa wakulima wetu na wananchi wetu ili tuwe na uelewa wa haya matakwa na ituwezeshe kuhakikisha kwamba tutakuwa tunazalisha mazao yanayoendana na itifaki husika ili tusije tukajikuta tumeridhia hili azimio, lakini hatujajengea uwezo wakulima na wananchi waweze kuzalisha, kusafirisha, kusindika na kuhifadhi kadiri ambavyo itifaki inahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba nirudie tena kwamba tunahitaji kuwa na Sheria ya Usalama wa Chakula; naomba nirudie tena, tunahitaji suala la usalama wa chakula liwe chini ya Wizara ya Afya; naomba nirudie tena, tunahitaji suala la usimamizi wa afya ya mazao ya kilimo yawe chini ya Wizara ya Kilimo; na kwa kumalizia tunahitaji wananchi wetu na wakulima wetu wajengewe uwezo juu ya hii itifaki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza kwa kuunga mkono hoja. Ningependa kumpongeza Mheshimwa Raisi kwa kupata billion 32 za kwenda kujenga upya soko la Kariakoo. Kimsingi soko lile linakwenda kutumiwa na wafanyabiashara ambao wanafanya kazi kwenye minyororo ya thamani ya sekta za uzalishaji kwa maana ya kilimo, mifugo na uvuvi. Hiyo inaendeleza azma ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha ya kwamba tunaimarisha hizi sekta za uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kunufaika na hizi sekta za uzalishaji, napenda kuishauri Serikali lazima tuwekeze kwenye mbegu kwa maana ya mbegu bora, hususani zitakazoweza kuhimili mabadiliko ya tabianchi. Lazima tuwekeze pia katika afya ya udongo wetu, lakini tatu lazima pia tuwekeze katika utafiti na huduma za ugani. Ili tuweze kufanya matatu yote haya lazima tuwekeze kwenye teknolojia na masuala ya TEHAMA, matumizi ya teknolojia kwa ajili ya kukuza kilimo na uzalishaji wetu na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hapa nirejee, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, mapema mwaka huu alisema kwamba tunakwenda kujenga kituo kikubwa cha TEHAMA hapa nchini. Kwa hiyo, hiyo inaonyesha dhamira yake kwenye masuala ya TEHAMA na kwenye Mpango huu ningependekeza Serikali ioneshe jitihada za makusudi kabisa, inakwenda kuinuaje sekta ya kilimo kwa kutumia teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kwenye mwezi wa Nane aliyekuwa Waziri wa Wizara inayosimamia masuala ya TEHAMA alisema kwamba Tanzania imepata dola miloni 150 kwenye mradi ambao unaitwa Tanzania Digital Project. Kwa hiyo ningependa kupendekeza baadhi ya zile fedha kama mgao ulivyofanyika kwenye hizi pesa za Covid, basi hata katika zile baadhi zielekezwe katika kufanya tafiti na kuja na ubunifu wa kiteknolojia ambao utatuwezesha kuwa na mbegu bora, kufahamu afya ya udongo wetu, lakini pia kutoa huduma za ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile hivi karibuni tumetangaziwa kwamba Benki ya CRDB imepata dola milioni moja kutoka kwenye Mfuko wa Mabadiliko ya Tabianchi ili kutoa mikopo kwa wakulima wadogo. Niiombe sana Serikali ihakikishe kwamba fedha zile zinakwenda kweli kwa wakulima wadogo na sio kunufaisha wafanyabiashara wakubwa, hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya zile fedha pia zinaweza zikaelekezwa katika kutafuta mbinu kwa kutumia teknolojia za kupambana na haya mabadiliko ya tabianchi ikiwemo narudia tena mbegu bora, kufahamu afya ya udongo wetu na kutoa huduma za ugani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeshasema kwamba ungependa kuona Bunge lako la Kumi na Mbili linaacha historia na legacy yake kwenye sekta ya kilimo. Wengi tumeongea kwamba tunahitaji bajeti iongezeke kwenye sekta ya kilimo, lakini tunayo fursa ambayo naiona ni low- hanging fruits. Kwenye sheria ambazo zipo chini ya TAMISEMI, kila halmashauri inatakiwa ifanye reinvestment kwa maana kwamba kama kwenye mapato ya council ilipatikana shilingi milioni moja kutokea kwenye sekta ya kilimo, wanatakiwa wafanye reinvestment asilimia 20 kwenda kukuza ile sekta ya kilimo. Asilimia 15 wafanye reinvestment kwenye sekta ya mifugo, asilimia tano kwenye sekta ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili la reinvestment halifanyiki. Kwa hiyo ni low-hanging fruits ambao sisi kama Bunge tunaweza tukahakikisha kwamba TAMISEMI watekeleze sheria hiyo, TAMISEMI watekeleza takwa hilo la kisheria, kwa sababu moja kwa moja hapo sekta ya kilimo itaweza kupata fedha nyongeza zinazotokana na uzalishaji kutokana na sekta hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuipongeza Serikali kwamba wamekuja na mpango wa e-commerce yaani biashara ya mtandao. Wanufaika wakubwa na biashara wa mtandao ni watu ambao wapo kwenye sekta za uzalishaji, kilimo, mifugo na uvuvi, lakini mpaka hivi sasa kwa mujibu wa taarifa za Shirikisho la Watoa Huduma za Simu - GSMA wanasema bado mpaka sasa asilimia 48 ya Watanzania hawatumii mobile internet. Sasa ikiwa bado hatutumii mobile internet ina maana hata matumizi yale ya e-commerce hatutaweza kufikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda nipendekeze kwa Serikali iwekeze jitihada kubwa kwa kushirikiana na wadau kuja na mfumo wa kuhakikisha kwamba wanatoa elimu ya digital literacy na digital skills, kwa sababu bila ya kufanya hivyo hata huu mpango wa biashara mtandao hatutaweza kunufaika nao kutoka na kwamba watu tunazo simu lakini hatutumii simu zetu kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia nielezee suala zima la vyanzo vipya vya mapato. Nakumbuka Mheshimiwa Raisi alivyokuja hapa kuhutubia kwenye Bunge lako Tukufu mwezi Aprili alisema kwamba tutanue wigo wa walipakodi. Hapa narudia tena kusema, lipo kundi kubwa la wafanyabiashara walio kwenye sekta isiyo rasmi. Katika kila shilingi kumi ambayo inazunguka kwenye uchumi wetu shilingi sita ipo kwenye sekta isiyo rasmi. Kwa hiyo, ni lazima Serikali ije na mpango mkakati wa namna gani tutarasimisha biashara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ningependa kupendekeza, ikiwa kama Serikali inaweze ikaweka mazingira wezeshi ya kuvutia wawekezaji, inaweza ikatoa misamaha ya kodi kwa ajili ya wawekezaji, kwa nini isifanye hivyo kuhakikisha kwamba inawavutia wale wajasiriamali ambao biashara zao hazijarasimishwa waweze kuzirasimisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana kuna swali liliulizwa kwamba tuna mabilionea wangapi? Kwa hivyo, ninachopenda kupendekeza ni Serikali ije na mpango wa kuweka angalau miaka miwili ya tax holiday, misamaha ya kodi kwa wazalishaji…

MWENYEKITI: Hivi tulijibiwa tuna mabillionea wangapi?

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tulijibiwa kwamba tuna mabillionea takriban 5000 na wote ni kwa hisani ya Chama cha Mapinduzi, kama nipo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwamba, tunahitaji kuja na mpango ambao utawavutia wale walio kwenye sekta isiyo rasmi kurasimisha biashara zao. Mpango ambao utawavutia vijana, wanawake na wenye ulemavu kuingia kwenye biashara rasmi. Kwa hiyo ningependa kuiomba Serikali ije na angalau miaka miwili ya msamaha wa kodi kwa biashara mpya ambazo zinaanzishwa na makundi haya na kama inafanya hivyo kwa wawekezaji naamini kabisa inaweza pia ikafanya hivyo kwa kundi hili la vijana, wanawake, watu wenye ulemavu na hapo ndio tutakuwa tunafanyia kazi ile dhana nzima ya kuongeza wigo wa walipakodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote hapa tunafurahia na tunamshukuru sana Mheshimiwa Raisi Samia Suluhu Hassan kwa pesa za Covid-19 ambazo zimeingia nchini. Pia ningependa kutumia fursa hii nipendekeze kwa Serikali iko haja ya kutumia makundi yenye ushawishi mkubwa kwenye jamii kumuunga mkono Mheshimiwa Raisi katika vita hii ya Covid-19 na kutoa elimu kwenye jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka siku ya Mkutano Mkuu wa NGOs, binafsi nilimwomba Raisi Samia Suluhu Hassan kwamba NGOs ziweze kushiriki kwenye kutoa elimu kwa jamii, wasanii washiriki kwenye kutoa elimu kwa jamii, vyombo vya habari vishiriki kwenye kutoa elimu kwa jamii, watu mashuhuri washiriki kwenye kutoa elimu kwa jamii kuhusu Covid-19, hata na sisi Wabunge tushiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningependa kuishauri sana Serikali, kama ambavyo Ofisi ya Rais, TAMISEMI wameweka wazi mgao basi na Wizara ya Afya pia iweke wazi mgao wa kile kipande cha elimu ya jamii kwenye upande mzima wa Covid-19, kwa sababu mpaka sasa hauelewi kipande kile kinatumikaje na nani ambaye anafanya au anatoa elimu hiyo ngazi ya jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile napenda kusisitiza sana iko haja kubwa ya kuweka kipaumbele kama ambavyo Wabunge wamesema katika Sekta ya Kilimo, Sekta ya Mifugo na Sekta ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga tena mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na mimi niungane na wenzangu kukupongeza sana kwa kupata nafasi hii na tunakutakia kila la heri katika kutekeleza majukumu yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia mimi nitajikita katika eneo la usalama wa chakula kwa maana ya food safety. Nasema hivi kwa sababu duniani kote masuala mazima ya usalama wa chakula kwa maana ya food safety yanaratibiwa chini ya Wizara ya Afya kwa maana ya kuwa chini ya mamlaka ya Kudhibiti Ubora wa Chakula na Dawa na hata Tanzania miaka ya nyuma ndivyo ambavyo tulikuwa tunafanya chini ya TFDA, na hata nchi za Afrika Mashariki zilikuja kwetu kujifunza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini miaka ya karibuni Serikali iliamua kuivunja TFDA na badala yake kuunda TMDA na jukumu la usalama wa chakula kwa maana ya food safety wakaliweka chini ya Shirika la Viwango (TBS). Sasa jambo hili mtaniwia radhi sana kusema lakini limeweka maisha na afya za watanzania rehani.

Mheshimiwa naibU Spika, nasema hivyo kwa sababu TBS ina jukumu la kuangalia ubora wa matairi, ubora wa mabati, ubora wa misumari mabati na kadhalika na hapo hapo iweje tena TBS hiyo hiyo ipewe jukumu la kuratibu na kudhibiti ubora wa usalama wa chakula kwa maana ya food safety.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa hawa TBS ndiyo wanaotoa vibali kwa wazalishaji wa chakula, halafu hao hao tena waende waangalie kama ule ubora kile kibali walichotoa kimekidhi, tayari hapo kuna conflict of interest.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo mahsusi ambalo lilijitokeza ambalo linadhihirisha kabisa TBS haiwezi kuendelea kubeba jukumu la usalama wa chakula kwa maana ya food safety. Mwaka jana kwenye tarehe 13 au 14 Oktoba, 2021 Shirika la Chakula na Madawa la Kenya lilitangaza kwamba linarudisha juice aina ya Ceres ya apple ambazo zilikuwa na aina moja ya sumukuvu ambayo ni hatari kwa maisha ya wanadamu. Mpaka siku hiyo kwa huku Tanzania TBS ilikuwa haijasema kitu chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, gazeti la Mwananchi likawatafuta TBS na nakumbuka Mkurugenzi mwenye Idara husika alisema kwamba mpaka muda ule wa kwenye tarehe 14 Oktoba juice aina ya Ceres ilikuwa haijaingia nchini na wanaendelea kufuatilia na pale ambalo zitaingia nchini basi watazizuia na watatoa taarifa na watafanya uchunguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku ya tarehe 16 Oktoba TBS ikatoa taarifa ya umma kuelezea kwamba wamejiridhisha juice zile hazijaingia nchini juice aina ya Ceres na barcode ambazo zilikuwa zimewekwa wakasema na waiambia umma kwamba kila kitu kiko sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa masikitiko makubwa TBS walitudanganya Watanzania kwa sababu kwenye tarehe 22 mimi kwenye kiosk kimoja hapa Dodoma nilikuwa zile juice za Ceres aina ya apple zikiwa zinauzwa na nilichukua jukumu la kupiga picha na kumtumia Waziri mwenye dhamana wa wakati ule wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ambaye akapokea akasema atalifanyia kazi. (Makofi)

Kwa hiyo, moja kwa moja inaonesha kwamba kwanza TBS hawachukulii serious jambo la usalama wa chakula kwa maana ya food safety; TBS hawana muda wa kuangalia masuala ya usalama wa chakula na TBS wanaendelea kuhatarisha maisha ya Watanzania kwa kuendelea kulimbikiza mambo mengi ambayo hayaendani pia na mambo ya usalama wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi kwa unyenyekevu mkubwa sana naiomba Serikali ipitie upya uamuzi wake wa kuondoa masuala ya usalama wa chakula kutoka Wizara ya Afya na kuyapeleka kwenye eneo la mambo ya Viwanda, Biashara na kadhalika turudi kwenye basic practice. Hii haitakuwa mara ya kwanza ya Serikali kufanya mapitio na maboresho ya uamuzi wake kadri ambavyo itaonekana inafaa.

Kwa hiyo, mimi kwa kumalizia na kwa unyenyekevu mkubwa sana na kwa maslahi mapana ya kulinda afya za Watanzania, kulinda mzigo mkubwa ambao Wizara ya Afya unao, kulinda mzigo mkubwa wa ongezeko kubwa la magonjwa ya kansa ambayo hayaeleweki, suala la usalama wa chakula kwa maana ya food safety lirudi ndani ya Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii, nami mchango wangu utajielekeza katika taarifa ya Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kutambua rasilimali watu tuliyonayo katika Diaspora, tumeona hivi karibuni ameendelea kutoa nafasi mbalimbali za uteuzi kwa Watanzania wenzetu ambao walikuwa wanafanya kazi nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo nipongeze Kamati kwa kutambua umuhimu wa Diaspora pia kwa kutambua kwamba bado hatuna mfumo sahihi wa kutambua wenzetu wa Diaspora lakini kuweza kuwafungamanisha katika maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narejea mwaka 2021 mwezi Juni nilichangia katika mchango wa bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje hapa Bungeni ilikuwa ni Tarehe 01 Juni, 202, ambapo niliishauri Serikali, kwakuwa suala la uraia pacha lina changamoto mbalimbali na linagusa Katiba, tujielekeza katika suala la Hadhi Maalum ambalo litawezesha diaspora kupata kila kitu na kunufaika na kujishughulisha na shughuli zote za kiuchumi, kasoro maeneo mawili. kujishughulisha na masuala ya kisiasa pamoja na ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama. Nashukuru wakati ule tulipata jibu hapa hapa Bungeni kwamba Serikali inafanyia mapitio Sera ya Mambo ya Nje, ndani ya Sera ile itaweka suala la diaspora na sera ile itakuwa tayari Disemba 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ni takribani miaka miwili toka Bunge la Bajeti 2021, mpaka leo hii bado Serikali haijaja hapa Bungeni kutueleza bayana ni lini itakamilisha mpango wa hadhi maalumu kwa ajili ya diaspora. Ninasema hivi kwa sababu mchango wa diaspora katika ukuaji wa uchumi kwa Taifa letu ni mkubwa sana. Kwa mwaka 2022 Kenya peke yake imepata dola bilioni nne kupitia Diaspora na imefikia mpaka Diaspora ndiyo wana mchango mkubwa zaidi kwa foreign currency katika nchi ya Kenya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tunahitaji rasilimali watu, tunahitaji rasilimali fedha, tunajaribu kukuza uchumi, tunao diaspora ambao wana taaluma kubwa, tunao diaspora ambao wana mitaji lakini kwa kuwa bado tunashindwa kutambua hadhi maalum na kukamilisha mchakato wake tunashindwa kunufaika na diaspora lakini na diaspora wanashindwa kunufaika na nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa muda mrefu katika safari zake za nje ya nchi na kila nchi anayokwenda anakutana na diaspora, ni mara kadhaa Mheshimiwa Rais amekuwa akiahidi diaspora kwamba suala la hadhi maalumu linafanyiwa kazi, sasa nashangaa sana kwa nini Wizara hii inakwamisha maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea Bungeni na kutueleza bayana suala la hadhi maalumu kwa ajili ya diaspora litakamilika lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha naomba sana nipate kauli ya Serikali ni lini itakamilisha mchakato wa wenzetu diaspora kupata hadhi maalum ili waweze kujishughulisha na shughuli za kiuchumi nasi kama Taifa tuweze kupata: -

(i) Takwimu sahihi za diaspora,
(ii) Takwimu sahihi za mchango wanadiaspora kwenye ukuaji wa uchumi wetu,
(iii) Kuwatumia katika rasilimali watu pale ambapo tunahitaki taaluma zao,
(iv) Kuwatumia katika rasilimali fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba sana Wizara hii iunge mkono jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kufungua uchumi wetu kidiplomasia na isiwe sehemu ya mkwamo wa kufanikisha suala la hadhi maalumu kwa diaspora. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Napenda kuanza kwa kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan, kwa dhamira yake ya dhati ya kuhakikisha anaweka mazingira wezeshi yatakayosababisha kufikia usawa wa kijinsia katika siasa hapa nchini kwetu Tanzania. Nasema hivi kwa sababu, ndani ya mwaka mmoia wa uongozi wake Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan, ameunda Kikosi Kazi cha Taifa ambacho kimepewa jukumu la kupokea maoni na kutoa ushauri juu ya hali halisi ya demokrasia ya vyama vya siasa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, na ninakumbuka kati ya vitu ambavyo amekuwa akisisitiza kwa kikosi kazi hiki ni kuhakikisha kwamba, wanaangalia pia kwa jicho la kipekee suala zima la usawa wa kijinsia kwenye siasa kuanzia kwenye vyama vya siasa vyenyewe. Nami nakubaliana kabisa na Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan juu ya umuhimu wa kufanya hivi kwa sababu, kwa mujibu wa Ripoti ya Uchaguzi Mkuu Tanzania ya Tume ya Uchaguzi NEC kati ya wagombea 11,933 waliogombea nafasi mbalimbali kuanzia Urais, Ubunge, Udiwani, katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015 ni asilimia 7.5 tu ndio walikuwa wanawake ilhali idadi ya wanawake waliojiandikisha kupiga kura ni asilimia 53 ya wapiga kura wote.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili. Takwimu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) zinaonesha pia asilimia kubwa ya wanawake waliopitishwa na vyama vyao kugombea nafasi mbalimbali za uchaguzi huwa wana fursa kubwa zaidi ya kushinda.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, mwaka 1995 CCM ilikuwa na wagombea wanawake saba kwenye majimbo na wanawake saba wote walishinda. Mwaka 2000 wanawake wa CCM ambao waligombea kwenye majimbo walikuwa 13 na kati ya hao 12 walishinda. Mwaka 2005 kulikuwa na wagombea wanawake 19 na kati ya hao 17 walishinda. Mwaka 2010 kulikuwa na wagombea 24 na kati ya hao wagombea 19 walishinda. Mwaka 2015 kulikuwa na wagombea 24 na kati ya hao 18 walishinda kwa upande wa CCM na kwa upande wa CHADEMA kulikuwa kuna wagombea 13 na sita walishinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii inadhihirisha kuwa wanawake wana uwezo mkubwa sana wa kushinda kwenye chaguzi endapo watateuliwa. Hivyo, dhamira ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kufikia usawa wa kijinsia inawezekana kabisa endapo tutaweka mikakati thabiti ya kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaeleza wazi kabisa kuwa binadamu wote ni sawa mbele ya sheria na kila mwananchi anayo haki ya kushiriki katika masuala ya umma, yakiwemo ya uongozi wa Taifa. Aidha, Sheria ya Vyama vya Siasa ya mwaka 1992 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2019 imegusia umuhimu wa vyama vya siasa kuzingatia masuala ya usawa wa kijinsia wanapotunga na kutekeleza sera zao, wanapoteua wagombea kwa ajili ya uchaguzi na uchaguzi wa viongozi ndani ya vyama.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na kwamba, sheria ya vyama vya siasa imeweka mazingira haya wezeshi, bado matakwa haya yanakuwa ni magumu kutekelezeka kwa sababu, yanamfanya Msajili wa Vyama vya Siasa anakosa meno ya kuvilazimisha vyama vya siasa vitekeleze usawa wa kijinsia. Kwa hiyo, ili tuweze kufikia dhamira ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kuwa na usawa wa kijisnia kwenye siasa, yapo mambo ya msingi ambayo lazima yafanyike. Kwa hiyo ningependa kuishauri Serikali yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Sheria ya Vyama vya Siasa liwekwe takwa la kisheria kwamba kila chama cha siasa kiwe kina sera ya usawa wa kijinsia. Jambo la pili, kama ambavyo kwenye Katiba na kama ambavyo kwenye Sheria ya Serikali za Mitaa pia kwenye Vyama vya Siasa viweke kiwango ambacho aidha kati ya asilimia fulani ya wagombea ambao watateuliwa na Vyama vya Siasa wawe wanawake. Vilevile katika mapato ambayo Vyama vya Siasa wanapata kupitia ruzuku, Vyama vya Siasa viweze kutenga kiwango fulani cha fedha ambacho kitakwenda kuwainua na kuwajengea uwezo na kuwasaidia wagombea wanawake.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni katika Sheria ya Uchaguzi huwa kunatokea matendo mengi ya ukatili wa kijinsia wa aina mbalimbali ikiwemo ukatili wa kimtandao pamoja na matusi na kufedheheshwa wakati wa kipindi cha kampeni wakati wa uchaguzi na hasa baada ya uchaguzi. Kwa hiyo, Sheria ile pia ya uchaguzi iweke wazi adhabu ambazo zitatolewa pale ambapo kutakuwa kuna udhalilishaji na ukatili wa kijinsia wa aina yoyote ile kwa wagombea wanawake. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Neema Lugangira kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Salome Makamba.

T A A R I F A

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Neema Lugangira kwamba, Sheria ya Uchaguzi inataka ujapofanyiwa makosa yoyote ya kimaadili upeleke kama ni kosa la jinai kwa sababu udhalilishaji wa kijinsia ni kosa la kijinai, unatakiwa upeleke kwenye mfumo wa kijinai ambao kiuhalisia inaweza ikachukua mpaka uchaguzi unaisha bado kosa lile halijafikiwa hatma. Kwa hiyo, nakubaliana naye kabisa kwamba Sheria ya Vyama vya Siasa na Sheria ya Uchaguzi iseme clear kama kumetokea kosa la jinai, basi mtu aliyemfanyia mwenzie kosa la unyanyasaji wa kijinsia apewe adhabu kupitia Kamati ya Maadili ambayo inasimamia uchaguzi na moja kati ya adhabu hizo ziwe strict iwe ni mtu huyo kuenguliwa katika kugombea.

Mheshimiwa Spika, nakubaliana nae kabisa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Neema Lugangira.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa kumalizia naomba kusisitiza na kuishauri, nashukuru sana naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili.

SPIKA: Ngoja. Mheshimiwa Neema mimi ndiyo naongoza kikao usiwasikilize hao wanakupoteza, kwa sababu mimi sijakuuliza kwa sababu yeye alichofanya hapo amechangia hajakupa wewe taarifa. Mheshimiwa Neema Lugangira malizia mchango wako.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa kumalizia napenda kusisitiza na kuishauri Serikali kwamba ilete ile Sheria ya Vyama vya Siasa na iifanyie maboresho ili Msajili wa Vyama vya Siasa aweze kuwa na meno ya kuvisimamia Vyama vya Siasa vyenyewe kutekeleza na kuimarisha na kufikisha usawa wa kijinsia kwenye siasa. Hii ni pamoja na kuhakikisha kwamba wanaweka angalau asilimia fulani ya wagombea katika nafasi zote za uchaguzi kuwa wanawake, pia Vyama vya Siasa viwe vina sera ya usawa wa kijinsia na vilevile katika Sheria ya Uchaguzi iweke wazi adhabu ambazo zitachukuliwa pale ambapo mgombea yeyote mwanamke iwe katika mchakato wa kampeni, uchaguzi na hata baadaye anapofanyiwa aina yoyote ya ukatili wa kijinsia, ikiwemo wa kimtandao ni hatua gani zitachukuliwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii nami naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Omari Kigua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza sana Serikali kwa jitihada za haraka ambazo imeshachukua, lakini naomba nasema kwamba jitihada hizi hazitaondoa taharuki iliyopo kwa sasa wala kupunguza mtikisiko wa kiuchumi ambao upo. Hivyo, ninapenda kuishauri Serikali mambo mawili yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ningependa tutambue kuna utofauti wa zile gharama ambazo zinachangia kupanda kwa mafuta kwa maana kwamba zipo kodi za Serikali na zipo kodi za kitaasisi. Kwa hiyo, mimi ningependa kujielekeza katika tozo za kitaasisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo napenda kuishauri Serikali ni kwamba tukiangalia tozo hizi za kitaasisi gharama yake inafikia karibu Shilingi 500. Kwa hiyo, nipendekeza kwa Serikali ione naomna gani ya kuondoa tozo hizi za kitaasisi na tozo hizi za kitaasisi haziathiri moja kwa moja mapato ya Serikali kwa maana ya kodi za Serikali, vilevile hazitagusa zile tozo ambazo zipo ringfenced kama maji pamoja na REA kwa maana ya umeme vijijini. Jambo hili linawezekana na hata hivi karibuni tutakumbuka kwamba Serikali iliondoa Shilingi 100 katika tozo hizi za mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo huo napenda kuishauri Serikali kwa msisitizo mkubwa ione namna gani ambavyo itaondoa tozo za kitaasisi ambazo zinakaribia gharama ya Shilingi 500. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, natambua kwa kuokoa...

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ninampa Msemaji Dada yangu Mheshimiwa Neema taarifa kwamba, pamoja na tozo hizi za kitaasisi, lakini kuna fedha ambazo zipo kwenye madini. Madini ambayo yamekuwa yakikamatwa kama faini sasa hivi ni wakati sahihi Serikali iuze, iweze kuingiza huku kama sehemu yakusaidia uchumi wetu ikiwa ni pamoja na zile dhamana zinazowekwa mahakamani, sasa hivi ziletwe ziingie huku. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha anayepewa taarifa yupo nyuma yako hapo.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, aahaa!

SPIKA: Haimaanisha uongee naye, ongea na mimi. (Kicheko)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, lakini la mwisho, fedha zile za CSR ambazo zinatolewa na Taasisi tunaweza tukaamua mwaka mmoja zote tuzichukue ziingie humu ziweze kutusaidia, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Neema Lugangira, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana naipokea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Spika, naendelea kusisitiza na kurudi palepale kujielekeza kwamba Serikali ione namna gani ya kuondoa tozo hizi za kitaasisi ambazo zinakaribia Shilingi 500 na jambo hili linawezekana na linaweza kufanyika kwa uharaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa pili kwa Serikali ni kwamba natambua baada ya tozo hizi za kitaasisi kuondolewa taasisi hizi zitakuwa na mapato mapungufu. Hivyo, Serikali itafute fedha za kuweza kutoa ruzuku au subsidy kwa hizi taasisi. Moja ya njia ambayo Serikali inaweza ikafanya ni kwa kuitisha vikao vya dharura na mashirika ya fedha yanayotudai yaani creditors wetu ili kujadiliana nao namna gani ambavyo tutaweza kupata kipindi maalum cha kutolipa yale makato ya mwezi. Tuweze kufanya loan repayment re-scheduling jambo ambalo linakubalika na katika majadiliano hayo Serikali iweze pia kuhakikisha ya kwamba kutakuwa hakuna penalty za aina yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mantiki hiyo, endapo tutafanikiwa katika jambo hilo basi ile fedha ambayo kila mwezi Serikali hivi sasa inatumia kulipa makato ya hii mikopo tuliyonayo ambayo ni takriban Bilioni 600 mpaka Bilioni 800 kila mwezi, fedha hiyo Serikali itaweza kutumia kuleta kwenye uchumi kama subsidy ili kupunguza makali ya kiuchumi na wananchi wote kwa ujumla tuweze kupata ahueni kutokana na janga hili la kiuchumi tulilo nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naamini kabisa Serikali sikivu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, itachukua ushauri wa Wabunge kwa uzito mkubwa na itaweza moja, kutoa tozo hizi za kitaasisi ili kupunguza gharama za mafuta. Pili, kuitisha mikutano ya dharura na mashirika ya kifedha yanayotudai ili kuona namna gani ambavyo tutaweza kufanya loan repayment scheduling. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa fursa hii, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii, nami nitachangia katika maeneo mawili; eneo la lishe shuleni na eneo la hedhi kwa maana ya watoto wakike kukosa shule kwasababu ya hedhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoongelea kuboresha elimu tunaongelea mambo yafuatayo: -

Mitaala jambo ambalo Serikali linaendelea nalo hivi sasa kwa hiyo nawapongeza, madarasa, madawati jambo ambalo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amelifanya kwa kiwango kikubwa na wote tumeshuhudia, vitabu, umeme, maji safi na salama, walimu, suala zima la TEHAMA shuleni tumesikia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba wanalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yote haya ili yaweze kuwa na tija ni lazima watoto wetu wanavyokuwa kwenye shule wapate chakula shuleni ni changamoto kubwa sana. Kwanza anafika shuleni hajala, halafu ashinde kutwa nzima shuleni akiwa anasoma huku akiwa na njaa. Wataalam wameshathibitisha kwamba njaa inamuathiri mtoto kuelewa, inamuathiri mtoto kuchanganua yale anayofundishwa na hatimaye inaathiri pia ufaulu wa watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna taarifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa WFP walikuwa wamefanya tathimini ya hali ya lishe kwenye shule duniani kote. Kwa hapa Tanzania ripoti yao ya mwaka 2020 ilionesha ya kwamba ni takribani watoto 500,000 mpaka 1,000,000 tu ambao wanapata uhakika wa lishe shuleni. Kwa maana hiyo idadi kubwa ya watoto bado hawapati lishe shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili nilichangia mwaka jana naninarudia tena mwaka huu. Ijapokuwa nawapongeza Wizara kwa kuzindua mwongozo wa lishe shuleni lakini mwongozo ule hauna mpango wa jinsi gani ambavyo utatekelezeka na wala mwongozo ule hauna bajeti ya namna gani ambavyo suala hili litatekelezeka.

Mheshimiwa Naibu spika, Kwa hiyo, mimi ningependa kuishauri Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; kama ambavyo Serikali inapanga mipango mbalimbali na kutafuta wadau kama vile Benki za Maendeleo na Wadau kutoka nchi za maendeleo wafanye hivyo pia katika hili eneo la lishe shuleni. Mwaka jana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alihutubia kwenye mkutano wa UN Food Systems kule New York. Moja ya matokeo ya mkutano ule ilikuwa ni kuanzisha kitu kinachoitwa school meals coalition. Na coalition ile inapanga kuhakikisha kwamba ifikapo mwaka 2030 kila mtoto kwenye shule atakuwa anapata angalau mlo mmoja wenye lishe bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana Desemba 2021 Global Partnership for Education (GPE) wametoa Dola milioni 580 kwa ajili ya kusaidia nchi za kutoka Barani Afrika kuimarisha lishe shuleni. Katika mpango huo Tanzania haijapata mgao.

Kwa hiyo, mimi ningependa kuwa challenge Wizara ya Elimu tuone namna gani na sisi tunanufaika kwenye haya maendeleo mbalimbali ya kidunia. Isitoshe mwenyekiti wa hivi sasa wa GPE ni Mheshimiwa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete. Kwa hiyo, kwa nini tusimtumie maana mwenyekiti wa mpango huo wa GPE ni Rais wetu mstaafu? Sisi Tanzania iweje hatunufaiki na jambo hilo? Desemba 2021 wametoa Dola milioni 580, nchi za wenzetu kama Nigeria nakadhalika wamepata Tanzania haijapata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vivyo hivyo tukija kwenye USAID in Foreign Aid kwenye upande wa agriculture kwenye Serikali ya Marekani mwaka 2021 wametoa Dola milioni 248 kwa ajili ya lishe shuleni, na kila nchi imepata Dola milioni 25 za kuimarisha lishe shuleni, Tanzania haijapata mgao, kwa nini? Na window ya hivi karibuni ya kuomba ufadhili huo USAID ilikuwa ni mei 6, 2022, wiki iliyopita tu; zote hizi ni grants. Kwa hiyo mimi niwaombe Wizara ya Elimu ibebe ajenda hii ya lishe kwa uzito mkubwa kwa sababu yote haya tunafanya ikiwa watoto hawafundishiki kwa sababu ya njaa tunafifisha jitihada kubwa za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa TAMISEMI kwenye kitengo chao cha lishe wanasema kwamba katika kila darasa la watoto 45, 15 hawafundishiki. Sasa kama 15 hawafundishiki kwanini baadaye tunakuja kulalamika ufaulu umeshuka tunalaumu mitaala, tunalaumu walimu ilhali watoto wetu wanashinda njaa hawana lishe shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakubaliana nami hata kipindi hiki cha Bunge tulipokuwa kipindi cha Ramadhani tulifupisha muda ili kukidhi, kwa sababu mtu ukishinda na njaa akili haiwezi kufikiri salama, sasa tunategemeaje watoto shuleni waweze kuelewa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi kwa mara ya pili tena na kwa masikitiko makubwa bado sijaona political will ya kutoka kwa Wizara ya Elimu kubeba ajenda ya lishe; hususani ukizingatia ajenda ya lishe ni moja ya ajenda za kipaumbele za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan tangu akiwa Makamu Rais na hata sasa akiwa Rais ameendelea kusemea umuhimu wa ajenda ya lishe. Kwa hiyo, mimi naomba sana Mheshimiwa Waziri atakapo hitimisha aje na mpango mahsusi wa kuhusu Serikali inapanga kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tunaimarisha lishe shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwenye eneo langu la pili. Mwaka 2021 NIMR wamefanya tafiti ya kuona ninamna gani ambavyo suala la hedhi linakosesha elimu watoto wetu wa kike. Kwa haraka haraka tafiti ile ilionesha watoto kuwa wengi wa kike hasa wa vijijini wanakosa shule kwa sababu yakuwa kwenye hedhi; na moja ya sababu ni kwamba hawawezi kumudu gharama za kununua pedi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi najiuliza; Wizara ya Elimu ina programu mbalimbali ambazo zinahusiana na masuala ya water sanitation and hygiene ambako jambo la hedhi linaingia pale, wanashindwa vipi kuingiza mkakati au kuja na programu ya kuhakikisha watoto wanaotoka kwenye kaya maskini wanapata taulo za kike ili wasikose shule kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika eneo hili naomba nipendekeze, kwamba tunayo TASAF ambayo ina jukumu la inahudumia kaya maskini; hivi kwanini kwenye TASAF tusiangalie, kwamba watoto wanaotoka kwenye kaya hizi maskini kuwe kuna intervention ya kuwawezesha wapate taulo za kike ili watoto hawa wa vijijini wanaotoka kwenye kaya maskini wasikose shule kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwezi mtoto anakosa siku tano mpaka saba kwa sababu ya kuwa kwenye hedhi, na Serikali imeweka jitihada kubwa ya kuhakikisha kwamba mtoto wa kike apate elimu, wakati jambo la kibailojia, jambo ambalo si sababu amesababisha yeye mwenyewe linamfanya akose shule akiwa kwenye hedhi.

Kwa hiyo, namuomba sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu, hii ni mara pili pia nachangia suala hili kwenye Bunge lako Tukufu, bado sijapata majibu yanayoeleweka kuhusiana na Serikali itakuja na mpango gani kuhakikisha kwamba mtoto wa kike hakosi shule kwa sababu ya hedhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi baada ya kusema hayo nasisitiza tena, kwamba Serikali ije na mpango wa kuhakikisha kuna lishe shuleni, Serikali ije na mpango wa kuhakikisha kwamba mtoto wa kike hakosi shule kwasababu ya hedhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana na endapo sitaridhika na majibu ya Serikali nitashika shilingi ya mshahara wa Waziri. Ahsante.
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia azimio hili la kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mtakubaliana nami katika kipindi hiki cha miaka miwili Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ameonesha wazi dhamira yake ya kusimamia misingi ya haki za binadamu, utawala bora, demokrasia, pamoja na diplomasia ya uchumi.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la haki za binadamu, nampongeza sana Mhehimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu mikutano ya hadhara, kufungulia vyombo vya habari vilivyokuwa vimefungwa, kukubali kufanya maboresho ya sheria za huduma za vyombo vya habari na tayari rasimu iko wazi, kusema hadharani kuhusu kutoridhishwa na upatikanaji wa Haki Jinai na kuunda Tume ya Haki Jinai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika katika eneo la utawala bora, nampongeza sana Mhehimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika hotuba yake aliyowasilisha wiki iliyopita kwenye Mkutano wa Summit for Democracy, ameiambia dunia kwamba Tanzania itarudi kujiunga katika OGP (Open Government Partnership). Hii ni hatua muhimu sana kwa sababu msingi wa OGP ni kuimarisha Serikali ambazo zinafanya kazi kwa uwazi, uwajibikaji na kuwainua wananchi kuweza kuwajibisha Serikali. Kwa kitendo hiki itaongeza imani kwa wawekezaji wakubwa ambao wanapenda kuwekeza kwenye nchi ambazo zina mifumo thabiti ya utawala bora na sera ambazo zinatabirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo la demokrasia, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuimarisha demokrasia hapa nchini kwetu. Alianza hivyo kwa kuunda kikosi kazi ambacho kimemshauri katika maeneo ya demokrasia ya vyama vingi vya kisiasa na mengi ambayo amependekeza, tayari ameshaanza kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikirejea tena katika hotuba yake ya wiki iliyopita katika Mkutano wa Summit for Democracy, Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameahidi kwamba Sheria ya Vyama vya Siasa inakwenda kuboreshwa, Sheria ya Taifa ya Uchaguzi inakwenda kuboreshwa na mchakato wa Katiba Mpya unakwenda kuanzishwa. Nami naamini kupitia yote haya, moja ya azma yake kubwa ya kuimarisha ushiriki na ushirikishwaji wa wanawake katika siasa na wenyewe utakwenda kuimarishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuhitimisha katika eneo la dipolmasia ya kiuchumi, wote mtakubaliana nami kwamba katika miaka hii miwili Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ameifungua nchi yetu. Katika kipindi cha miaka miwili, kupitia ziara alizofanya nje ya nchi, tumeweza kupata miradi yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 793 ambayo imesajiliwa TIC. Hilo ni jambo kubwa sana la kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vivyo hivyo, hivi karibuni tumepata ugeni wa Makamu wa Rais wa Marekani Mheshimiwa Kamala Harris, na kupitia ugeni wake Tanzania imeweza kupata msaada wa kifedha wa jumla ya Dola za Kimarekani milioni 560 ambayo ni sawasawa na takribani shilingi trilioni 1.3.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, inaonesha ni namna gani ambavyo kuna umuhimu mkubwa wa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan aendele kufanya ziara nje ya nchi kwa sababu ziara hizi zinapata tija na sisi ambao tunapata nafasi mbalimbali za kushiriki mikutano ya nje ya nchi, tunajisikia fahari sana pale ambapo tunajitambulisha tunatoka Tanzania. Nasi tunafuata nyayo zake za kuhakikisha kwamba fursa yoyote ambayo tunaipata tunaisemea vizuri nchi yetu na tunatafuta fursa mbalimbali za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja na naomba niungane na Wabunge wenzangu wote na Watanzania wote kumuunga mkono na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa mageuzi makubwa anayoyafanya katika eneo la haki za binadamu, eneo la utawala bora, eneo la demokrasia na eneo la diplomasia ya uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii. Napenda kuanza kwa kumshukuru kwa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri na Wizara ya Kilimo kwa kutambua umuhimu wa lishe. Kwa mara ya kwanza kwenye hotuba ya bajeti ya Wizara ya Kilimo jambo la lishe limetambuliwa na limetajwa kwa kina. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo, hivi karibuni Wizara ya Kilimo imezindua Kampeni ya Kitaifa ya Lishe na huo ni mwendelezo wa kutekeleza ahadi ya Ilani ya Chama vha Mapinduzi ambapo jukumu la kutokomeza masuala ya udumavu na aina zote za utapiamlo yamewekwa chini ya Wizara ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru sana pia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweka uzito mkubwa katika suala zima la tafiti na uzalishaji wa mbegu ili kuongeza tija ya kilimo. Nami mchango wangu kwa siku ya leo utajikita katika eneo la mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri wa Kilimo amesema, “hivi sasa tunazalisha mbegu kwa asilimia 26 tu ya mahitaji yetu.” Kwa maana hiyo, bado uzalishaji wa mbegu uko chini na hatujitoshelezi. Kwa hiyo, lazima tuweke jitihada za makusudi kabisa ili kuongeza uzalishaji wa mbegu hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake ameelezea mipango ya kina ya Serikali katika kufanya tafiti na pia kuimarisha mbegu za msingi pamoja na mbegu za awali. Naomba nitumie fursa hii kuikumbusha Wizara Kilimo, hatuwezi kuongeza tija ya mbegu zetu kama hatukuwa tunajumuisha mbegu za asili. Kwa mantiki hiyo, namshukuru pia Mheshimiwa Waziri ametoa ahadi hapa kwamba ifikapo 2025 mbegu za asili zitakuwa zinauzwa madukani kama ilivyo mbegu nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tufikie hapo, yapo mambo ya msingi lazima yaanze kufanyika hivi sasa. Kwa hiyo, napenda kupendekeza mambo manne yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, tukija kwenye suala la kiusalama, tumeona vita ya Ukraine na Urusi, jinsi ambavyo nchi inaweza ikaamua kutokuuzia kile ambacho inazalisha. Kwa hiyo, nasi tukiendelea kutegemea mbegu za nje kwa zaidi ya asilimia 70, ipo siku tutakuwa hatarini kutopata mbegu yoyote, hivyo kujikuta tuna njaa. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri ahakikishe ya kwamba suala la uzalishaji wa mbegu ndani ya nchi analitia uzito mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili, Sheria ya Mbegu ya Mwaka 2003 haitambui mbegu za asili. Sasa tutafikaje 2025 kuzizalisha ziuzwe madukani ikiwa Sheria ya Mbegu ya Mwaka 2003 haitambui mbegu za asili? Kwa hiyo, naomba sheria hii ya mbegu ya mwaka 2003 ifanyiwe mapitio ili sheria hii izitambue na iweze kuzilinda mbegu zetu za asili kama ambavyo wanafanya nchi za wenzetu India, Ufilipino, Malaysia, Ethiopia na Zimbambwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa tatu, ni lazima sasa Wizara ichukue jitihada za makusudi kabisa za kuboresha Kituo cha Tafiti cha Kutumia Vinasaba vya Mbegu ili kwanza kuimarisha uzalishaji wa mbegu zetu na pia sisi kama Taifa tunaweza tukaingia kwenye soko la vinasaba vya mbegu duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa mwisho, ni lazima tuanzishe benki ya mbegu za asili ambazo zitasimamiwa na jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naungana na wenzangu kuwapongeza sana Waziri Mheshimiwa Bashe pamoja na Mheshimiwa Anthony Mavunde. Mheshimiwa Bashe ni kaka yangu, ni kati ya mentors wangu, lakini atakapohitimisha, asiponipa maelezo ya uhakika ya kujitosheleza kwamba Wizara hii inakwenda kufanya nini ili kuzitambua na kuzilinda mbegu za asili, basi nitaondoka na Shilingi yake na ataifuata Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria na naomba nianze kwa kutambua na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa ya kuimarisha eneo zima la haki za binadamu, demokrasia pamoja na utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sanjari na hayo napenda kufanya rejea kwenye mchango wangu katika bajeti hii ya Wizara Katiba na Sheria ambayo nilitoa mwaka jana Tarehe 28 Aprili, 2022 ambapo nilipendekeza ya kwamba Serikali ilete Bungeni Sheria ya Vyama vya Siasa pamoja na Sheria ya Uchaguzi ili zifanyiwe maboresho kwa lengo zima la kuimarisha ushiriki wa wanawake kwa maana ya usawa wa kijinsia katika siasa lakini pia kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanawake ndani ya vyama vya siasa na vivyo hivyo kutambua suala zima la ukatili wa kimtandao kwa wanawake wanasiasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Damasi Ndumbaro ambaye aliridhia mapendekezo hayo na akaielekeza Tume ya Kurekebisha Sheria ibebe jukumu hilo na ianze kufanya mapitio ya sheria hizo mbili, nami nilipata fursa ya kukutana na Tume hiyo na kuwasilisha maoni yangu siku ya Tarehe 11 Mei, na naipongeza sana Tume ya Kurekebisha Sheria kwa sababu natambua ya kwamba, mwezi wa Tatu mwaka huu wamewasilisha ripoti ya mapendekezo yao kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hivyo naipongeza sana Kikosi Kazi cha Mheshimiwa Rais waliopewa jukumu la kutoa maoni na mapendekezo kuhusu hali nzima ya masuala ya demokrasia ya vyama vingi vya siasa hapa nchini, ambao na wao wameshawasilisha ripoti yao kwa Mheshimiwa Rais waliwasilisha mwishoni mwa mwaka jana, nami pia nawashukuru kwa kunipa fursa ya kuwasilisha maoni yangu mbele ya kikosi kazi hicho siku ya Tarehe 14J ulai, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huu naomba nitumie fursa hii kuishauri na kuiomba Serikali kwamba itakapoleta maboresho ya sheria hapa Bungeni ya Sheria ya Vyama vya Siasa pamoja na Sheria ya Uchaguzi yafuatayo yazingatiwe: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, Sheria ya Vyama vya Siasa na Sheria ya Uchaguzi itakapoletwa iainishe bayana namna ambavyo uteuzi wa wagombea ndani ya Vyama vya Siasa utafanywa na itapendeza sana iwapo sheria hii itakamilika na kuletwa Bungeni kabla ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka kesho 2024. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu, kwa takwimu za sasa ni asilimia 2.1 tu ya Wenyeviti wa Vijiji ambao ni wanawake asilimia 12.8 tu ya Wenyetivi wa Serikali za Mitaa ambao ni wanawake asilimia 6.7 tu ya Wenyeviti wa Vitongoji ni wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni dhahiri kwamba bado ipo haja ya kuongeza idadi ya viongozi wanawake katika hizi nafasi za kisiasa. Kwa muktadha huo, lazima Sheria ya Vyama za Siasa pamoja na Sheria ya Uchaguzi zije Bungeni kabla ya mchakato mzima wa kuteua wagombea kwa ajili ya Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili; katika mchakato wa Katiba mpya, naiomba sana Serikali ihakikishe kwamba asasi za kiraia kwa maana ya CSOs na NGOs zishirikishwe ipasavyo. Moja, zishirikishwe katika kutoa elimu kwa umma kuhusu Katiba; pili, zishirikishwe katika kutoa mchango na maoni katika namna bora ya kuboresha Katiba mpya. Hapa nitilie mkazo, ni muhimu sana kuhakikisha asasi za kiraia kwa maana ya CSOs na NGOs za mikoa ya pembezoni nazo zinashiriki ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa tatu ni kuhusiana na Samia Legal Aid Campaign. Naipongeza sana Serikali kwa kuja na Samia Legal Aid Campaing, lakini nitumie fursa hii kusisitiza kwamba Samia Legal Aid Campaign ijielekeze zaidi katika changamoto ambazo zinawakumba wanawake na watoto. Mathalani, matunzo kwa watoto, ukatili wa kijinsia, mirathi, ardhi na mengineyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo huo, asasi za kiraia kwa maana NGOs na CSOs zipate fursa ya kushiriki katika maeneo yao. Hapa kipekee na kwa upendeleo kabisa naiomba sana Serikali kupitia Wizara hii, kwamba kwa kuwa Kagera ni kati ya mikoa ambayo ina changamoto kubwa katika maeneo haya, basi katika ile mikoa mitano ya mwanzo ambapo Samia Legal Aid Campaign itakwenda kufanyika, na Mkoa wa Kagera uwe mmojawapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe kwa kusemea viongozi wa Serikali za Mitaa. Nimefanya utafiti mdogo katika majimbo yetu na Wabunge wa majimbo wapo hapa ndani ya Bunge; iko changamoto kubwa ambayo inaendelea kwamba Mwenyekiti wa Kijiji au Mwenyekiti wa Serikali za Mitaa, au Mwenyekiti wa Kitongoji anaweza akaondolewa katika nafasi yake bila kufuata utaratibu unaostahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali, itakapoleta hapa Bungeni Sheria ya Uchaguzi, ihakikishe Sheria hii inawalinda Viongozi wa Serikali za Mitaa waweze kumaliza muhula wao kama ambavyo sheria hii inalinda Madiwani na Wabunge. Pale ambapo kutakuwa na hitaji la kumwondoa kiongozi yule, basi kuwe na utaratibu ulio wazi, unaoeleweka ili kuondoa mianya ya hivi sasa ambayo inaweza kupelekea mtu kufanyiwa hila, mtu kutotendewa haki na kuondolewa pasipo utaratibu sahihi. Siyo hivyo tu, kuna suala zima la haki ya kuchaguliwa na haki ya kuchagua. Hivi sasa yako maeneo mengi ambayo yanaongozwa na aidha Wenyeviti wa Vijiji, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa kwa maana ya Wenyeviti wa Mtaa au Wenyeviti wa Vitongoji ambao wanakaimu. Hili jambo siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali ihakikishe kwamba inaweka utaratibu wa kulinda viongozi wetu wa Serikali za Mitaa kama ambavyo Madiwani na Wabunge wanavyolindwa, na pale ambapo kutakuwa na haja ya kumwondoa, basi uwekwe utaratibu rasmi kwa maana ya kufuata vigezo ili impeachment iweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa fursa. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hoja hii muhimu ya hotuba ya bajeti ya Wizara ya Afya. Niungane na Wabunge wenzangu kuipongeza sana Wizara inayoongozwa na dada yangu mahiri kabisa Mheshimiwa Waziri Odo Ummy Mwalimu, lakini pia na Naibu Waziri Dkt. Mollel na viongozi wote wa Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa naendelea kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kusisitiza kwamba kwenye Wizara hii ya Afya pamoja na kufanya tiba, lazima tuwekeze jitihada za maksudi kabisa kwenye kinga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi za Wizara nikiri wazi nimesikitika kwamba katika hotuba nzima ya Mheshimiwa Waziri na baada ya kusikiliza hotuba pia nimeipitia, sijasikia akigusia jambo lolote linalohusiana na suala zima la usalama wa chakula. Nasema usalama wa chakula kwa maana ya food safety. Mara kadhaa ndani ya hili Bunge tumekuwa tukisisitiza suala la usalama wa chakula ni dhamana ya uhai na maisha na afya ya Watanzania. Hatuwezi kuendelea kuweka maisha ya Watanzania rehani kwa kuruhusu suala la kudhibiti usalama wa chakula kwa maana ya food safety iendelee kuwa chini ya TBS kwa maana ya Wizara ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri TBS ina conflict of interest. Huwezi ukawa wewe ndio unatoa vibali kwa wafanyabiashara, halafu wewe ndio unaangalia udhibiti wa usalama wa chakula kwa maana ya food safety. Mheshimiwa Waziri ni shahidi pamoja na Naibu Waziri, hili jambo nimelisemea mara nyingi hata nikiwa kwenye Kamati ya Huduma ya Maendeleo ya Jamii iliyokuwa Huduma ya Maendeleo ya jamii na hata ndani ya Bunge lako Tukufu. Tukifanya rejea kwenye hansard tutakuta kuna kauli ya Serikali kupitia Wizara ya Afya ambayo iliahidi kwamba Serikali inafanyia kazi jambo la kuhamisha mamlaka ya masuala ya usalama wa chakula, kutoka kwenye TBS na kuja kwenye Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa, pamoja na pongezi na jitihada kubwa za Sekta hii ya Afya kumekuwa na ongezeko kubwa la magonjwa ya kansa, kumekuwa na ongezeko kubwa na magonjwa yasiombukiza ambayo hayaeleweki, ambayo mengi yao yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na ulaji wa vyakula ambavyo havina ubora wa usalama wa chakula. Ikiwa tunaweza kukidhi vigezo vya usalama wa chakula ili tupate soko la nje. Kwa mfano soko la EU, tunashindwa vipi kulinda na kukidhi na kuweka vigezo vya kulinda uhai wa soko la ndani ambalo ni zaidi ya wananchi milioni 60. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala naongea kwa uchungu mkubwa kwa sababu tunaendelea kuweka maisha ya Watanzania rehani, wakati tunaweza kudhibiti ikiwa tu tutarudisha mamlaka ya udhibiti ya usalama wa chakula yarudi chini ya Wizara ya Afya, ambao kimsingi ndiyo awna dhamana ya kuhakikisha uhai wetu unaendelea kuwa salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana viongozi wa Hospitali zetu za KCMC, Bugando, Muhimbili, JKCI, Ocean Road, hapa Benjamini Mkapa, lakini naamini hata na wao watakubaliana nami, suala la usalama wa chakula limekuwa likiendelea kutotiliwa mkazo na maanani wakati linaendelea kutuwekea Watanzania hatarani. Haiwezekani tukaendelea kuruhusu suala la usalama wa chakula kwa maana ya food safety libaki chini ya TBS ambao kimsingi mimi binafsi ninao ushahidi dhahiri na nimeshasema hapa Bungeni. Kuna ndugu yangu aliwahi kuagiza bajaji, bajaji zile zilikwenda kufanyiwa ukaguzi na wahitimu wa food science, kwa nini? Kwa sababu pale TBS hawana kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anafanya kazi kubwa sana, nimwombe sana atulinde Watanzania, tunaingiza vyakula hapa nchini, nani anaangalia usalama wa vyakula vinavyoingia. Tunazalisha chakula hapa nchini, nani anaangalia usalama wa chakula tunachokula? Nani anaangalia machinjioni usalama wa chakula, nani anaangalia mbogamboga na vyakula vinavyokuja sokoni iwapo chemical residue yake ipo vipi, lakini tunafanya hivyo kwa soko la nje, kwa nini tunashindwa kufanya hivyo kwa soko la ndani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ina maana wale wananchi wa nje wana haki zaidi kuliko sisi Watanzania zaidi ya milioni 60.

Pamoja na kwamba dada yangu nampenda sana, niweke wazi nisipopata kauli ya Serikali inayoridhisha kuhusu nini Serikali inakwenda kufanya kuhusu suala zima la kuhakikisha usalama wa chakula kwa maana ya food safety linarudishwa kwenye Wizara ya Afya, naondoka na shilingi ya mshahara wa Waziri mpaka kieleweke.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa fursa hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hoja ya hotuba ya bajeti ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum. Kwanza kabisa ningependa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Dkt. Dorothy Gwajima pamoja na Naibu Waziri, Mwanaidi na viongozi wote wa Wizara hii kwa kazi kubwa ambayo wanaifamnya.

Mheshimiwa Spika, natambua jitihada za Bodi ya Uratibu wa NGOs chini ya uongozi mahiri wa Mama yangu Mheshimiwa Mwantumu Mahiza pamoja na jitihada za Ofisi ya Msajili wa NGOs katika kuhakikisha kwamba NGOs zote ambazo zinasajiriwa hapa nchini zinafanya kazi kwa kile ambacho wamekiombea lakini pia kwa kufuata mila tamaduni na desturi zetu.

Mheshimiwa Spika, aidha, napenda pia kutumia fursa hii kuwasihi sana viongozi wa dini, viongozi wa kisiasa pamoja na viongozi wa Serikali ngazi ya jamii na katika maeneo yetu yote waweke jitihada ya kuhakikisha kwamba tunazitambua NGOs ambazo zifanya kazi katika maeneo yetu ili nasi tuwe sehemu ya mabalozi wa kuhakikisha ya kwamba NGOs kwenye maeneo yetu wanafanya kazi kulingana na mila tamaduni na desturi, ikiwemo yale ambayo walisajiriwa nato.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutambua mchango mkubwa wa NGOs katika maendeleo ya jamii. Na kipekee nakishukuru tena chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa kutambua umuhimu wa mchango wa mchango wa NGOs na hata kupelekea kutenga nafasi zake mbili za viti maalum kwa ajili ya NGOs ndani ya Bunge lako Tukufu. Niko mimi nawakilisha NGOs kwa upande wa Tanzania Bara lakini yupo pia na Dada yangu Mheshimiwa Khadija Aboud ambaye anawakilisha NGOs kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti hii mimi nitajielekeza kwenye maeneo matatu, eneo la kwanza ni local content kwenye sekta ya NGOs. Lazima tuweke jitihada za makusudi kabisa kuhakikisha kwamba NGOs za ndani zinaweza kunufaika na miradi mbalimbali inayoingia nchini pamoja na ufadhiri. Kwa takwimu za Ofisi ya Msajiri wa NGOs kwa mwaka jana jumla ya tirioni 1.1 zimeingia na kuratibiwa kupitia NGOs hapa nchini; lakini cha kusikitisha asilimia 70 imepita kwenye NGOs za nje kwa maana za kimataifa na ni asilimia 30 tu ambayo imepita kwenye NGOs za ndani kwa maana ya NGOs za Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, mimi ningependa kupendekeza kwa Serikali kuputia Wizara hii waone namna ya kuweka mwongozo ambao utaratibu vizuri, kwamba fedha zinapoingia Tanzania kwa ajili ya miradiya maendeleo ngazi ya jamii lazima NGOs za ndani zipewe kipaumbele. Hiyo itasaidia moja, kuhakikisha kwamba NGOs zetu zinafanya kazi kwa kuzingatia mila tamaduni na desturi, lakini pili kuhakikisha kwamba NGOs zetu zinaweza kukua na miradi inakuwa endelevu.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo ningependa kuzungumzia ni kwamba bado kuna sintofahamu kubwa katika sekta ya NGOs na masuala mazima ya kikodi. Natambua kwa upande wa sekta binafsi wanayo kamati ya maboresho ya sera za kodi, yaani wanaita thick tank, ambayo mara nyingi sekta binafsi inakaa na Wizara ya Fedha na Mipango na wanajadili changamoto mbalimbali za kikodi na wanazipatia ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, Mimi ningependa kupendekeza kupitia Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum sekta ya NGOs iweze kupata kamati ya kikodi ambayo itakuwa inakaa inajadiliana na Wizara ya Fedha na Mipango kuhusu changamoto za kikodi na kupata utatuzi wake.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ambalo ningependa kulichangia katika eneo hili ni kwamba, kuna umuhimu mkubwa sana wa NGOs kushirikishwa katika mipango mbalimbali ya Serikali Wizara hii inagusa masula ya jinsia masuala ya wanawake ambapo masula ya uongozi na ushiriki wa wanawake katika siasa ni moja ya majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, kama ambayo tunatambua Serikali inakwenda kufanya maboresho ya Sheria za Vyama vya Siasa, Sheria za Taifa za Uchaguzi na hata pia mchakato wa katiba mpya. Mimi niombe sana Wizara hii kupitia Mheshimiwa Waziri kuhakikisha kwamba katika michakato ya sheria hizo NGOs zinashiriki ipasavyo lakini pia katika mchakato wa katiba mpya NGOs si tu zinashiriki lakini pia zinawakilishwa ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuhitimisha, naomba niwapongeze tena Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya lakini niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu na Watanzania tutambue mchango mkubwa ambao unafanywa na NGOs ngazi ya jamii kwa sababu NGOS ndizo ambazo zinashirikiana na Serikali kufikisha huduma pale ambapo Serikali haiwezi kufika, kufikisha maendeleo pale ambapo Serikali haiwezi kufikisha, kwa hiyo ni muhimu tufanye kazi kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, lakini naendelea kusisitiza pia sisi kama viongozi na viongozi wa dini viongozi wa kisiasa viongozi wa kiserikali lazima nasi pia tuwe tunajukumu la kuhakikisha ya kwamba NGOs hizi zinafanya kazi kwa matakwa ya sheria zetu, Katiba yetu mila tamaduni na desturi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuhitimisha, nasisitiza tena umuhimu wa kuwa na Kamati ya kikodi baina ya Sekta ya NGOs na Wizara ya Fedha na Mipango ili tuweze kuhakikisha tunatatua changamoto za kikodi zilizopo. Nasisitiza umuhimu wa kuhakikisha kwamba Serikali inakuja na mwongozo ambao utapelekea NGOs za ndani ziweze kupata rasilimali fedha kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hoja hii ya bajeti ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Mheshimiwa MNami napenda kuungana na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dokta Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anafanya mageuzi makubwa ya teknolojia na maendeleo ya kidijitali hapa nchini kwetu, ikiwemo pia kuhakikisha kwamba Serikali inaboresha namna ambavyo inafanya kazi kwa kutumia TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Nape Nnauye na Viongozi wote wa Wizara hii kwa mageuzi makubwa ambayo anaendeleea kuleta katika sekta hii muhimu. Kipekee ningependa pia kumpongeza sana Dada yangu Justina Mkurugenzi Mtendaji wa UCSAF kwa kazi kubwa ambayo anafanya, siyo tu ya kupeleka minara lakini ya kuhakikisha ya kwamba shule zetu zinaunganishwa na mtandao ili watoto wetu waanze kukua kupata elimu ya kidijitali na stadi zingine tokea wakiwa kwenye umri mdogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo awali kulikuwa hakuna Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na badala yake masuala yote yanayohusiana na TEHAMA yalikuwa yamegawanywa ama yametapakaa sehemu mbalimbali kwa maana ya Serikali, taasisi na maeneo mengine ya Serikali. Kwa utashi wa Mheshimiwa Rais Dokta Samia Suluhu Hassan mwaka 2021 aliamua kuunda Wizara hii mahsusi ambayo itakuwa na mamlaka na dhamana ya kusimamia na kuunganisha na kuratibu masuala yote yanayohusu na TEHAMA na ninampongeza sana Mheshimiwa Rasi kwa jambo hilo kwa sababu limeongeza tija ambayo wengi wetu tunaisifia hapa leo Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya badiliko hilo, moja ya vitu ambavyo vilifanyika ni kuhamisha Data Center ambayo ilikuwa iko chini ya Ofisi ya Rais na ikahamishiwa ikaletwa kwenye Wizara hii. Lengo zima ni kutimiza lengo la Serikali kuwa na sehemu moja ya kukusanya data na ilionekana kwa kuwa sasa tuna Wizara hii mahsusi, basi jukumu hilo liletwe kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika mchango wangu wa siku ya leo nitajikita katika e-GA (E-government Agency). E-government Agency hivi sasa iko chini ya Ofisi ya Rais, Utumishi na ninatambua kwamba chini ya e-GA kuna sehemu mbili. Sehemu moja ni platform, sehemu nyingine ni masuala ya utumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kupendekeza ya kwamba suala la utumishi libaki kwenye Ofisi ya Rais, Utumishi lakini suala la e-GA platform lihamishwe liletwe kwenye Wizara hii ambayo ndiyo ina dhamana na mamlaka ya usimamizi wa masuala yote ya TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu hivi sasa ijapokuwa tunayo e-GA lakini kutokana na pale ambapo ipo, hivi sasa kuna mifumo mingi ambayo haisomani. Nitatoa mfano mdogo, Walimu wetu ambao wako chini ya TAMISEMI wanatumia mifano mingi kuingiza taarifa na mifano hiyo haisomani.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu tukija kwenye sekta ya afya. Leo hii mimi naweza kufanya kipimo cha CT scan Hospitali yetu ya Benjamin Mkapa hapa Dodoma lakini nikilazimika kufanya CT scan Muhimbili Dar es Salaam, inabidi nifanye CT scan tena kwa sababu mifumo haisomani na viko vipimo hivi vya afya ambavyo huruhusiwi kufanya mara kwa mara.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba tumepongeza maeneo mengi yamepata minara lakini kwa masikitiko makubwa kwa Wilaya ya Nyang’hwale hakuna mnara hata mmoja na taarifa tulizileta kwamba kuna tatizo la usikivu. Kwa hiyo, nataka nikupe taarifa kwamba tunapongeza lakini Wananyang’hwale tuna masikitiko makubwa. Ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Amar umesimama hiyo ndiyo hoja aliyokuwa anazungumza Mbunge kweli? Mheshimiwa endelea.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba utanilindia muda wangu. Kama nilivyokuwa nasema kuna umuhimu mkubwa wa mifumo hii kusomana kwa sababu pasipo kusomana inawaongezea gharama kubwa sana Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa hapa kwenye eneo hili, digital competitiveness ya nchi yaani ushindani wa kidijitali wa nchi unapimwa kutokana na ushiriki wa startups kwa maana ya sekta binafsi. Kwa kuwa e-GA iko chini ya Ofisi ya Rais, Utumishi, e-GA wanafanya mifumo yote wenyewe, hawashirikishi hata kidogo sekta binafsi wala startups zetu, wakati hapa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ninampongeza sana nimefarijika kusikia lengo la Wizara ni kuona namna gani ambavyo tutaimarisha startups zetu ili nasi tuweze kufika mahali startups zetu ziweze kuuza nje ya nchi teknolojia yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tunasifika kwa mfumo wa GePG (Government Procurement) na mfumo wa BRT (Mabasi ya Mwendokasi) lakini nchi zinakuja kujifunza hapa kwetu, kitakachokuja kutokea sasa ni nchi hizi zitajifunza kwetu, zitapeleka haya kwenye sekta binafsi yao, wale watatengeneza halafu wale watauza watanufaika kwa kile ambacho kilanzia kwetu. Hili jambo lazima tuliangalie kwa jicho la kipekee na kwa wivu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haraka nitatoa mfano mdogo wa nchi kama Estonia. Nchi ya Estonia ina watu milioni 1.3 tu lakini inasifika katika startups zao kuja na teknolojia ambazo zimeweza kuvuka mipaka. Wana startups 10 na hizi startups 10 peke yake zina thamani ya zaidi ya Dola bilioni moja. Hiyo ndiyo dhana nzima ya kuwa na masuala haya ya e-GA na masuala ya ubunifu kwenye Wizara ya TEHAMA. Kwa hiyo, mimi naendelea kusisitiza kwamba Serikali ione namna ya kuhamisha masuala ya e-GA kutoka ilipo na yaje kwenye Wizara hii ya TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo tu hivyo, kwa kuwa e-GA inafanya biashara peke yake inaiongezea gharama kubwa sana Serikali. Nitatoa mfano mdogo uko Mfumo wa TANePS. Huu mfumo umetumia takriban zaidi ya shilingi bilioni sita na bado haujakamilika. Huu mfumo ungepewa kwenye sekta binafsi ingetumika takribani chini hata ya shilingi bilioni moja na mfumo ungekuwa umeshakamilika. Kwa hiyo mimi ambacho ningependa kumuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake anipe kauli na maoni na mipango ya Serikali, kwa kuwa sasa tunayo Wizara mahususi, Wizara hii ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia na Habari atuambie nini mpango wa Serikali katika kuhamisha suala la e-GA kwa upande wa platform litoke Ofisi ya Rais, Utumishi na lije kwenye Wizara hii mahsusi ili tuweze kupata tija lengwa na tuweze kuimarisha ushindani wetu wa kidijitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye hoja hii ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani. Kwanza kabisa ningependa kuipongeza sana Serikali kupitia Mheshimiwa Rais, Doctor Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa ambao Serikali inaendelea kufanya kwenye Jeshi la Zimamoto. Tarehe 22 Mwezi wa Tano nikiwa pale Bukoba tulipata ajali la moto kwenye Soko letu la Bukoba na kipekee niwapongeze sana Wanabukoba wenzangu pamoja na Jeshi la Polisi na Jeshi la Zimamoto kwa kazi kubwa waliyoifanya kuhakikisha ya kwamba moto ule unazimwa kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo yote yaliwezekana kutokana na uwekezaji mkubwa ambao umeendelea kufanyika kwenye Jeshi la Zimamoto. Kipekee namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, maana Serikali imeshatuma shilingi milioni 600 ambazo zinalenga kujenga kituo cha zimamoto kwa pale Bukoba na kituo hiki kitajengwa katika Kata ya Miembeni pale Bukoba Mjini. Kwa hiyo nami kama Mjumbe wa Kamati hii ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama naendelea kuafarijika sana kwamba yale ambayo tunayashahuri yanafanyiwa kazi na uwekezaji mkubwa unaendelea kufanyika kwenye Jeshi letu la Zimamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu katika bajeti hii utakuwa katika maeneo matatu na nitaanza kwanza katika eneo la idadi ya mahabusu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya ya kuhakikisha kwamba tunapunguza msongamano kwenye magereza yetu ikiwemo; moja, kutoa maelekezo kwamba mtu asipelekwe mahabusu mpaka upelelezi uwe umekamilika lakini pili, kuunda Tume ya Haki Jinai. Pamoja na hayo hivi sasa kwa takwimu za jana idadi ya mahabusu ni 12,012 na Serikali inatumia takribani milioni 640 kulisha mahabusu hawa kila mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, milioni 640 kila mwezi zinaenda kulisha mahabusu hao ambao hawafanyi kazi hivyo hawawezi kuzalisha chakula ambacho wanakula. Asilimia kubwa kati ya hawa ni petty offenders kwa maana ya kwamba ni wale wenye makosa madogo madogo yenye dhamana lakini dhamana hiyo inakuwa haipatikani. Ili tuweze kuhakikisha kwamba tunaweza kupunguza msongamano kwenye magereza yetu, mimi napenda kupendekeza mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo napendekeza, Wizara itupe taarifa tokea Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan alivyotoa maelekezo kwamba mtu asiende mahabusu mpaka upelelezi umekamilika. Je jambo hilo limefanyika kwa kiwango gani? Ni muhimu sana tupate taarifa kamili ya utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Jeshi la Magereza lifanye tathmini wale mahabusu ambao wako nao 12,012 kati yao ni asilimia ngapi ya mahabusu hao wana makosa yale madogo madogo yenye dhamana kwa maana ya petty offenders.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa tatu ni kwamba kumekuwa na changamoto kubwa kwamba mtu anakaa mahabusu kwa miaka mingi takribani miaka miwili, mitatu, mwaka na kadhalika lakini pale ambapo hukumu yake inatolewa ule muda aliokaa mahabusu hauhesabiki kama sehemu ya kifungu. Jambo hilo badala yake limeachiwa utashi wa Jaji ama yule ambaye anatoa hukumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitarejea hivi karibuni Mfalme Zumaridi kule Mwanza, Jaji alivyotoa hukumu yake alitoa maelekezo kwamba sehemu ambayo ameshakaa mahabusu iwe ni sehemu ya kifungo na baada ya kauli hiyo kilichofanyika yule Mfalme Zumaridi alikaa magereza mwezi mmoja tu, kwa sababu ule muda ambao alishakaa mahabusu ulihesabika lakini jambo hili haliko uniform. Jambo hili linategemea wengine wanapata wengine hawapati, jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa nchi yetu, kwa sababu inaweza ikaleta vurugu na wale ambao wako mahabusu wakajiona kwamba kuna wengine wanahaki zaidi kuliko wenzao. Kwa hiyo, mimi napendekeza kuwe kuna uniformity.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ni hapo kwenye suala la kupunguza msongamano wa magereza, napendekeza ya kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani ije na Mswada wa Sheria ya Dhamana (Bail Act). Kwa sababu hivi sasa masuala ya dhamana ni kifungu kimoja tu katika sheria ya Mwenendo ya Mashauri ya Jinai (The Criminal Procedures Act) na ni kutokana na hivyo kumekuwa na mkanganyiko na loop holes nyingi ambazo zinapelekea kuchelewesha haki ya dhamana na haki jinai kwa ujumla wake. Kwa hiyo, mimi napendekeza Wizara hii ituletee Muswada wa Sheria ya Dhamana kwa maana ya Bail’s Act.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa eneo langu la pili nitaongelea suala zima pale Mkoani kwetu Kagera kwenye Magereza ya Bukoba. Tuseme mahabusu au magereza ambao wanaumwa ambao wanapata rufaa ya kuja hospitali ya Mkoa wanawekwa kwenye lile Gereza la Bukoba na wengine wanapata Rufaa kwenye Bugando, lakini Gereza la Bukoba halina gari la kuwasafirisha wafungwa hawa na mahabusu pale ambapo wanaenda kupata matibabu, badala yake wanawasafirisha kwenye magari mengine, magari ya kawaida pamoja na raia. Kwa kipekee sana naomba Wizara ione namna gani ambavyo itapatia Magereza ya Bukoba Mjini iweze kupata gari ili iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho kutokana na miundombinu ya Mkoa wetu wa Kagera na hali ya hewa naomba sana Mkoa wa Kagera uangaliwe kwa jicho la kipekee, ili tuweze kupata magodoro, blanketi na sweta za kutosha. Maana hivi sasa katika magereza zetu nane za mkoa wa Kagera tuna takribani wafungwa na mahabusu zaidi ya 1900 na lakini tuna upungufu wa magodoro masweta na mablanketi kwa zaidi ya 15,000. Kwa hiyo, naamini sana kupitia ombi hili Magereza za Mkoa wa Kagera zitapata kipaumbele pale ambapo Jeshi la Magereza litaweza kutoa vifaa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na naipongeza sana Wizara, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Hamad Masauni, Mheshimiwa Naibu Waziri Sagini kwa kazi kubwa ambayo wanafanya na Viongozi wote wa vyombo vya Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika Bajeti Kuu ya Serikali, na nianze kwa kutambua na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kuinua uchumi wa Tanzania pamoja na uchumi wa mtu mmoja mmoja. Aidha, kipekee ningependa kumpongeza sana na kumtia moyo mchumi mbobezi kabisa, Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba na Wizara yake nzima kwa kazi kubwa wanayofanya, na kazi yao tunaiona na kupitia bajeti hii tuna ona dhamira ya dhati kabisa ya kufanya uchumi wa Tanzania upae.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia haraka haraka kwenye maeneo matatu. Eneo la kwanza, naishukuru sana Serikali kwa kuyafanyia kazi maoni ambayo sisi Wabunge tunatoa, maana nafahamu Serikali ilitambulisha kodi ya huduma za kidigitali na kampuni za nje kama Facebook yaani meta wameshaanza kuwasilisha taarifa zao Serikalini, nawapongeza sana. Aidha, nawapongeza pia kwa uamuzi wa kuamua kutoza kodi kwa biashara za mitandao (online businesses) kwa maana halisi ya online businesses ambazo hazina maduka sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitoe tu angalizo kuhusu kutoa kodi kwa hawa watu wanaoitwa influencers. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, tuwe na definition sahihi ya influencer ni akina nani. Kwa sababu mathalani mimi naweza nikawa ni shabiki wako, nika-post kazi inayokuhusu wewe lakini utakuwa hujanilipa, mimi nimefanya tu kwa utashi wangu na kwa namna ambavyo ninakukubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hapa pia nimeona viongozi wengi pamoja na Wizara nyingi zimelipia kwenye Kampuni ya Twitter ili wapate verification. ambapo wanalipa gharama kwa dola nane mpaka kumi kwa mwezi. Sasa ningependa kufahamu pia Wizara ina mpango gani wa kupata kodi kupitia fedha inayolipwa Twitter kupitia viongozi wetu wa Serikali pamoja na Wizara husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili; Serikali ilishaweka dhamira ya dhati ya kuona namna gani ambavyo tunainua uchumi wa mwananchi mmoja mmoja hususan makundi maalum kupitia wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Hii imefanyika kupitia sheria ya manunuzi, ya asilimia 30. Ningependa kupata kauli ya Mheshimiwa Waziri nini ambacho anapanga kufanya ili kuhakikisha kwamba wanawake, vijana na makundi maalum wananufaika na asilimia 30 ya manunuzi ya umma kama ambavyo Sheria ya Manunuzi ya Umma imeelekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho, dhamira ya dhati ya Serikali ni kuinua uchumi wa nchi yetu, na ili tufanye hivi ni lazima Serikali iweke jitihada za makusudi kabisa kuangalia mikoa ambayo inatambulika kama ina hali kubwa ya umaskini ilhali ni mikoa ambayo haipaswi kuwa katika nafasi hiyo. Hapa nitaongelea Mkoa wangu wa Kagera. Mkoa wa Kagera umepakana na nchi tatu, umepakana na Rwanda, Burundi na Uganda na unabeba asilimia kubwa ya Ziwa Victoria. Una hali nzuri ya hewa, una ardhi yenye rutuba, unapata mvua misimu miwili na zaidi kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapaswa ije na mkakati thabiti wa kuona namna gani ambavyo itainua uchumi wa Mkoa wa Kagera, kwa sababu kwa hali ilivyo sasa haikubaliki na hairidhishi. Kwa hiyo kwa haraka haraka ningependa kushauri maeneo yafuatayo kuhusiana na kuinua uchumi wa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, ulikuwepo mradi wa Mto Ngono, na naishukuru Serikali wameshaanza kufanya upembuzi yakinifu. Lakini mimi naona na ninaomba sana Serikali mradi huu uwekwe katika orodha ya miradi ya kielelezo (flagship project) na uweze kutafutiwa wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, kwa kutambua kwamba Mkoa wa Kagera unapakana na nchi tatu na fursa zilizopo katika ukanda huo wa nchi za maziwa makuu, niombe sana Serikali irudishe mpango wa kujenga airport ya kimataifa, maana mpango ulikuwepo. Wakati sasa umefika tuurejeshe mpango ule ili Mkoa wa Kagera upate airport ya kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo tunayo Airport ya Bukoba, wengi tunafahamu mchango wa Airport yetu ya Bukoba, niombe sana Serikali katika mwaka huu wa fedha ambao tunakwenda, 2023/2024, Airport yetu ya Bukoba iweze kufanyiwa uwekezaji kupata fog light pamoja na control tower ili safari za kwenda Mkoani Kagera ziwe ni safari zisizo kuwa na misukosuko na ikiwemo pia kufungua uchumi wa Mkoa wetu wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, natambua kwamba Wilaya ya Bukoba Mjini ndiyo reception ya Mkoa wetu wa Kagera unaounganisha Mkoa wetu na nchi zinazo tuzunguka. Naomba kipekee kabisa Stendi ya Bukoba Mjini ipewe kipaumbele katika Mkoa wetu wa Kagera ikiwemo pia na Soko Kuu. Haikubaliki kwamba Mkoa wetu kwa namna ulivyo na kwa ukubwa wake, na ukizingatia hata kitakwimu za sensa tunazaidi ya watu milioni tatu lakini mpaka leo Stendi yetu haieleweki ni lini itajengwa na fedha kupangwa ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoelekea kumalizia, Mkoa wa Kagera una zaidi ya ranch tano lakini bado ranch hizi hazijaonesha katika umahsusi wake unachangia vipi katika biashara ya nyama ikiwemo pia biashara ya maziwa. nikuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kwa kushirikiana na Mawaziri wenzako mfanye tathmini, na hili jambo hata Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alishalisema. Tufanye tathmini ya zile ranch nini kifanyike ili ranch hizi ziwe na tija ziweze kuchangia ukuaji wa uchumi si tu wa Mkoa wa Kagera lakini na uchumi wa Tanzania. Ili ranch zile wapewe wawekezaji ambao wataleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami naunga mkono hoja, na ninaendelea kumpongeza sana Mwanauchumi Mbobezi Daraja Moja Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Wizara yako nzima. Halikadharika namshukuru sana na ninampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya, ahsante. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, niungane na wenzangu kuipongeza sana Wizara hii chini ya uongozi mahiri kabisa wa Mheshimiwa Nape Nnauye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada kubwa sana ambayo Wizara hii inafanya katika kuhakikisha kwamba inaimarisha upatikanaji wa huduma wa mtandao wa internet bado kuna changamoto kubwa ya upatikanaji wa huduma ya internet hususani katika maeneo ya pembezoni kama vile Kigoma, Kagera, Mtwara, Lindi, Tanga pamoja na Mikoa ya Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kutambua hilo, napenda kuishauri Wizara itambue mbinu mbadala ya kufikisha huduma ya internet Vijijini ikiwemo na Mikoa yote ya pembezoni. Na njia hii ni kutumia community networks. Nchi za wenzetu kama Uganga, Kenya, Zimbabwe, Afrika Kusini wamenufaika sana kwa kutumia community networks kufikisha huduma ya internet kwenye shule pamoja na Vituo vya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa unyenyekevu kabisa, ningependa kuiomba Wizara kufanya mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, chini ya TCRA Wizara itambue kundi hili la community networks.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, chini ya TCRA Wizara itambue kundi hili la community networks. Jambo la pili, Wizara ipunguze gharama za Bendipana kwa community networks (broadband costs). Jambo la tatu, Wizara iondoe co-location fee kwa community networks. Yaani unakuta community networks wakitaka kuweka vifaa vyao kwenye minara ya UCSAF wanachajiwa gharama. Kwa hiyo, Wizara iondoe gharama hiyo kabisa kwa ajili ya community networks pale ambapo watataka kuweka vifaa vyao kwenye minara ya UCSAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne, Wizara itoe msamaha kwa hizi community networks kuchangia katika kapu la Mfuko wa Mawasiliano yaani UCSAF kwa sababu kimsingi community networks hazifanyi biashara, kimsingi community networks zinatoa huduma ya kijamii ili kuwezesha shule pamoja na vituo vya afya vya vijijini na mikoa ya pembezoni iweze kuunganishwa na huduma ya internet. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo langu la pili, naipongeza sana Wizara pamoja na UCSAF kwa kazi kubwa inayofanya ya kuimarisha mawasiliano hapa Tanzania. Pamoja na hayo, naomba niseme kwamba, wakazi wa Bukoba Mjini, Mkoani Kagera wanapata shida kubwa ya mawasiliano yasiyokuwa na uhakika hususan upatikanaji wa mtandao. Naweza nikasema katika kati ya Kata 14 za Bukoba Mjini, Kata nane za greenbelt zinapata changamoto kubwa ya mtandao wa uhakika; Kata hizi ni Buhembe, Nyanga, Kahororo, Nshambya, Ijuganyondo, Kagondo, Kibeta na Kitendagulo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa unyenyekevu mkubwa kabisa, ningependa kumwomba Mheshimiwa Waziri, baada ya Bunge hili la Bajeti afike pale Bukoba Mjini ajionee kero kubwa ya mawasiliano ambayo tunaipata. Hapa ningeomba atakapokuja na dada yangu jembe kabisa Mkurugenzi Mtendaji wa UCSAF, dada Justina na yeye afike, aone namna gani ambavyo atatusaidia kuimarisha mawasiliano pale Bukoba Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka, naendelea kuipongeza Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya kwenye anuani ya makazi. Hata hivyo, jambo hilo la anuani ya makazi linaleta changamoto kubwa ya kiusalama, usalama wa taarifa zetu binafsi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aharakishe utaratibu wa kuleta Sheria ya Data Protection hapa Bungeni ili tuweze kuipitia na kuipitisha ili kulinda taarifa zetu binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa natambua zipo Asasi za Kiraia ambazo zimeshaanza mchakato huu, kwa mfano, Jamii Forum na wengine na tayari ipo rasimu ambayo imeandaliwa. Kwa kazi iliyobaki ni ndogo, Wizara ichukue jitihada ambazo zimeshaanza ilete Sheria ya Data Protection hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni mtumiaji mkubwa sana wa mitandao ya kijamii, naamini anaona namna gani ambavyo wanawake wanasiasa hususan Wabunge wanawake tunavyopitia ukatili mkubwa wa kijinsia mtandaoni. Jambo hili lipo kwenye Wizara yake, nimwombe Mheshimiwa Waziri atafute namna ya kutulinda kwenye mitandao ya kijamii; kwanza kwa kuhakikisha kurasa zetu za mitandao zinapata verification ili kutuondoa katika hatari ya kudukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nashukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye hii Finance Bill. Kwanza kabisa napenda kuanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuja na bajeti ya kimkakati ambayo inalenga kwenda kuinua uchumi wetu na hata uchumi wa mwananchi mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuanza kwa kuchangia kwenye eneo la Part 24 Amendments ya Value Added Tax Act ya 2014 Cap. 148, ambapo kwenye ukurasa wa 42 Serikali imeridhia ombi ambalo mimi binafsi nilitoa pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine ya kuacha msamaha wa VAT kwenye bidhaa za taa zinazotumia nishati ya jua kwa maana ya solar lights. Jambo hili litakwenda kuwasaidia sana wananchi wetu hususani wananchi wa vijijini, ili waweze kuendelea na shughuli zao za kujiinua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hapa, napenda kupendekeza kwa Serikali kwamba kwa kuwa bado upatikanaji wa maji haujasambaa maeneo yote nchini, basi Serikali iweze pia kutoa msamaha wa kodi kwenye pump za maji zinazotumia solar (solar water pumps). Hii itasaidia sana: moja, kufanikisha ile kampeni ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kumtua mama ndoo kichwani na pia itasaidia kulinda watoto wetu ambao wengi wanapata changamoto mbalimbali wanapokwenda visimani kuchota maji; na tatu, itasaidia katika kilimo cha mboga mboga, matunda na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili hili katika ukurasa wa 43 chini ya kipengele hiki cha Part 24, Serikali pia imesikia kilio cha wadau wengi wa mazao haya ya mboga mboga, matunda na maua ambapo imeweka msamaha wa kodi wa cold rooms. Hili ni jambo jema sana ambalo litakwenda kuimarisha biashara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kupendekeza Serikali katika eneo hili, iongeze pia zile cold trucks, kwa sababu hivi sasa kuna changamoto kubwa ya kusafirisha haya mazao.

Nikitoa tu mfano mdogo wa samaki, unakuta mara nyingi hata ukiwa Mkoa wa Dar es Salaam unakuta sSamaki zimerushwa nyuma ya pickup, zinapigwa jua yaani haziko katika mazingira salama, zinakaa kwenye foleni muda mrefu na changamoto kubwa unakuta cold trucks bado kodi yake ipo juu. Kwa hiyo, kwa muktadha ule ule ambao Serikali imeweka msamaha wa kodi kwenye cold rooms, basi naiomba Serikali pia ifanye hivyo kwenye hizi cold trucks. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, naomba niende kwenye Part 10 ya Amendments ya Local Government Finance Act Cap. 290 kwenye ukurasa wa 15. Hapa Serikali imependekeza kwamba, makampuni yalipe Service Levy peke yake na yasilipe produce cess. Hili ni jambo jema sana, lakini kuna athari kwamba linaweza likapunguza mapato ya Halmashauri, hususan pale ambapo produce cess ni kiwango cha juu zaidi ya Service Levy.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningependa tu kuikumbusha Serikali kwamba chini ya sheria hii kuna takwa la kisheria ambalo linasema kwamba kila Halmashauri inatakiwa ifanye re-investment kwenye sekta ya kilimo, sekta ya mifugo na sekta ya uvuvi kulingana na yale mapato yake ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kama kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri, Halmashauri inatakiwa i-reinvest asilimia 20 kwenye sekta ya kilimo, asilimia 15 kwenye sekta ya mifugo na asilimia 5 kwenye sekta ya uvuvi. Jambo hili toka sheria hii ilivyotungwa, yaani toka takwa hili lilivyowekwa kwenye sheria hii, halijawahi kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano mdogo kwa haraka, Halmashauri ya Mufindi mapato yake ya ndani ni shilingi bilioni tatu kati ya hizo bilioni tatu shilingi bilioni 2.4 zinatokana na sekta ya kilimo, lakini halmashauri hii ina re-invest kwenye kilimo asilimia mbili tu ambayo ni milioni 60 wakati ilitakiwa ili-invest asilimia 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo tukija kwenye Halmashauri ya Njombe mapato yake ya ndani ni bilioni 1.5. Kati ya hiyo milioni 600 zinatokana na sekta ya kilimo lakini ina re-invest asilimia mbili tu ambayo ni milioni 12 wakati sheria hii inataka kwamba re-invest asilimia 20. Kwa hiyo kwa kuwa Serikali imeamua kwamba makampuni yasilipe produce cess yalipe tu service levy. Basi niiombe Serikali iweke mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba halmashauri zinatenga fedha za re-investment kama ambavyo sheria hii imeagiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la faini za bodaboda na bajaji. Serikali kwa nia njema imepunguza faini kutoka elfu 30 mpaka elfu 10. Malengo makuu ya hizi faini huwa ni matatu; la kwanza ni kumfanya aliyefanya kosa ajifunze; kufanya wengine wasifanye kosa; kuzuia mtu asifanye kosa. Sasa kwa kupunguza kutoka elfu 30 mpaka elfu 10 tunafifisha haya malengo ya faini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kupendekeza kuwa, Serikali ije na mfumo wa kuweka point system kwenye hizi leseni. Kwamba humu mwendesha bodaboda au bajaji akifanya kosa la kwanza atalipa elfu 10 sawa; akifanya kosa la pili alipe elfu 10 sawa; akifanya kosa la tatu kulingana na ile point system, basi leseni yake ifungiwe. Kwa sababu kwa kufanya hivyo ndiyo tutaendelea pia kulinda ile dhana nzima ya zile faini na kulinda watumiaji wa zile pikipiki na bajaji, lakini hata na maisha ya wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana; tusiache hii faini ya elfu 10,000 peke yake, Serikali ije na point system ambayo itasaidia kuhakikisha kwamba huyu dereva wa bodaboda au bajaji, akishalipa faini zake mara tatu basi akae akijua kwamba leseni yake imefungiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema kwamba, nakiri na natambua nia njema ya Serikali ya kuimarisha vyanzo vyake vya mapato kupitia sekta ya kilimo. Hata hivyo, napenda kuishauri Serikali kwamba mwaka wa fedha ujao, hebu Serikali ije na vyanzo vipya vya mapato ili tusiendelee kukamua kundi lile lile badala yake tuangalie makundi mengine ambayo hivi sasa hayatozwi kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa napenda kurejea ushauri ambao niliutoa. Naiomba sana Serikali ije na utaratibu wa kutoza kodi ya huduma za kidigitali yaani digital service tax. Kwa sababu kwa kufanya hivyo Serikali itaweza kupanua wigo wa walipa kodi badala ya kuendelea kutoza kodi nyingi zaidi kwenye kundi lile lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)