Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Deus Clement Sangu (29 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia hotuba zote za Mheshimiwa Rais, kwanza kabisa ikiwa mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako tukufu, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijaalia kuweza kufika mahali hapa. Lakini kwa namna ya pekee wananchi wa Jimbo la Kwela kwa kuniamini kuwa Mbunge wao, naomba niwahakikishie nitawatumikia kwa nguvu zangu zote na uwezo wangu kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijaalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mchango wangu nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa namna alivyowasilisha hotuba nzuri sana alipolihutubia Bunge hili la Kumi na Mbili. Kuna mambo mengi mazuri yameelezwa katika hotuba hiyo, lakini mimi kwanza nianze na sekta ya madini. Kweli tupongeze hasa alivyoitendea haki kwa miaka mitano iliyopita ambayo sasa sekta ya madini imeweza kuchangia Pato la Taifa. Kutoka mwaka 2015 ilikuwa ni 3.4% na sasa sekta ya madini inachangia Pato la Taifa kwa 5.2% ni mafanikio makubwa yanastahili pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika hotuba yake Mheshimiwa Rais aliongelea jambo kubwa sana na kuutangazia ulimwengu juu ya kuvumbua kwa gesi ya helium ndani ya Bonde la Ziwa Rukwa. Gesi hii inaenda kuleta mapinduzi makubwa katika uchumi wa Tanzania, lakini naomba nitoe rai na juzi nilikuwa nateta na Naibu Waziri wa Madini akanihakikishia kwamba mwezi nne zoezi la kufanya inflation na drilling inaweza ikaanza, changamoto ninayoiona ni maandalizi. Mara nyingi tunakuwa na miradi mikubwa kama hii kwa mfano hii gesi ya helium wasiojuwa ni gesi yenye thamani kubwa na Tanzania tuna ujazo unaokaribia futi za ujazo bilioni 1.38 ambao tunawazidi hadi nchi ya Marekani mara mbili na ambao uchimbaji wa gesi hiyo wao mwaka huu inaelekea kufikia ukomo. Kwa hiyo sisi kama Tanzania tutakuwa tunaweza kuongoza soko hilo la dunia na kuweza kuilisha dunia kwa miaka 20 ijayo na jambo hili liko kwenye Bonde la Ziwa Rukwa ndani ya Jimbo langu la Kwela kuna hekta 3,500. Maandalizi ninayosema ni kuandaa wananchi maana yake huu mradi unaweza kwenda kwao wakaupokea kama tu muujiza kwa kuwa hawakuandaliwa yakatokea mambo kama yale yaliyotokea Mtwara.

Pili, miundombinu naona bado si rafiki sana, nadhani Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi wewe ni shahidi siku ya mwaka mpya tulikuwa ndani ya eneo hilo ninalolisema ulijionea hali ya miundombinu ya barabara kuwa ni mibovu, sasa tuna mradi mkubwa kama huu, miundombinu ya barabara ni mibovu kiasi kile na hata Mheshimiwa Waziri Mkuu ni shahidi mwaka juzi ulikuja kule Bonde la Ziwa Rukwa ulijionea mpaka ukaanza kuuliza kuna njia nyingine tutarudi tena tulikotoka, lakini njia ndiyo hizo hizo Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Kwa hiyo, niombe tunapokuwa na mradi mkubwa tufanye maandalizi mazuri ili huu mradi uweze kuleta manufaa makubwa kwa taifa lakini kwa watu wale ambao wanaishi maeneo yanayozunguka mradi mkubwa kama huu.

Mheshimiwa Spika, pili nichukue nafasi hii kuongelea sekta ya kilimo na naomba hapa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu mnisikilize kwa makini. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais ameeleza wazi kwamba tunaagiza ngano kutoka nje karibu tani 800,000 kila mwaka, lakini nitangaze neema ndani ya Bunge lako tukufu, ndani ya Mkoa wa Rukwa tuna ekta zipatazo zaidi ya 60,000 ambazo zimefanyiwa tafiti na zinafaa kwa kilimo cha ngano. Tukiwekeza huko hakika hata hizi shortage ya tani 800,000 itakuwa historia. Tayari Mkoa wa Rukwa hasa katika Jimbo langu la Kwela eneo hilo lipo, nakuomba Mheshimiwa Waziri wa kilimo na Naibu Waziri kama mtaweza yeyote atakayeweza afike huko twendeni mkajionee jambo hili na pia tuitumie Benki ya Maendeleo ya Kilimo kwa maana ya Benki ya Kilimo waje waweze kuwawezesha wananchi ili hii shortage ambayo inatokea, sisi tumeumizwa sana, tumelima kwa nguvu kubwa, mahindi tumezalisha tani nyingi, tumebaki nayo majumbani yanaoza na mwaka huu tumelima sana hatujui tutapeleka wapi walau hii ujio wa ngano hii na sisi tutapata ahueni kama mkoa na kuachana sasa tuanze kugawa tulime nusu mahindi na nusu ngano kwa sababu mahindi yametutesa, hatujui wapi kwa kupeleka na hali ni nguvu pamoja na hayo uzalishaji huu tunaofanya unategemea tu mvua, umwagiliaji miradi mingi tuliyonayo hasa kwenye Jimbo langu ime-prove failure.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya hasa ndani ya jimbo langu la Kwela.

Mheshimiwa Spika, pili nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri unayoifanya, hasa kwa ziara yake aliyoifanya jimboni Kwela mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia kwa njia ya maandishi kwenye bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu; kwanza nianze kwa kumkumbusha Mheshimiwa Waziri Mkuu juu ya ahadi yake aliyoitoa siku alipofanya ziara Jimboni kwangu, juu ya ujenzi wa hospitali yenye hadhi ya wilaya katika Mji Mdogo wa Laela ambao pia ndio Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiodhihirika kwamba Hospitali ya Wilaya iliyojengwa kwenye jimbo langu ipo umbali wa zaidi ya kilometa 330 ambapo imekuwa ngumu kufikiwa na wananchi hasa waliopo Ukanda wa Ufipa ya Juu ambao ni takribani wananchi 200,000.

Mheshimiwa Spika, pia naomba nichangie kuhusu mgogoro wa ardhi uliopo kati ya mwekezaji wa shamba la Malonje yaani Efatha Ministry. Mgogoro huu umechukua muda mrefu sana. Nilisema humu Bungeni mwaka jana na Serikali ikaahidi kuchukua hatua, lakini mpaka sasa hamna hatua yoyote. Nikuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu utusaidie ili tuweze kumaliza tatizo hili lililochukua muda mrefu.

Lakini pia mgogoro wa Gereza la Mollo lililopo Wilaya ya Sumbawanga na wananchi wa Kata ya Msanda Muungano juu ya kukabidhiwa ekari 495 walizoahidiwa na Waziri wa Mambo ya Ndani alipozuru eneo hilo. Lakini ni mwaka wa tatu sasa hamna hatua yoyote iliyochukuliwa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya kukabidhi ardhi hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii niweze kutoa mchango wangu kwenye sekta hii muhimu ya Kilimo. Ndugu yangu Mheshimiwa Bashe, nikupongeze umetoa hotuba nzuri ya bajeti ya kilimo na mwelekeo kwa ajili ya bajeti inayogusa watanzania walio wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa namna ambavyo amekuwa akitupia jicho kwenye Wizara hii. Kwa kweli kwa jinsi tulivyokuwa tukipitia bajeti ya Kilimo kwa miaka ya nyuma na kuanzia mwaka 2022/2023 wa bajeti Mheshimiwa Bashe, huna kisingizio chochote, imebaki tu sisi kukupigia kelele Wizara ya Fedha ikuletee fedha na mwaka huu pia naona bajeti imeongezeka kwa asilimia hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nikupongeze ulifanya ziara ndani ya Mkoa wa Rukwa na hususani ndani ya Jimbo langu la Kwela, kwa mara mbili mfululizo. Leo, nilijua unakuja ku–table bajeti yako hapa, kuna mambo uliahidi kule jimboni katika ziara zako zote mbili. Kwa hiyo, nilitumia wikiendi hii kufanya ziara maeneo yale uliyoahidi ndani ya Jimbo la Kwela. Nikupongeze kweli mambo yote uliyoniahidi, uliahidi utaanza upembuzi yakinifu kwenye scheme 11 ndani ya zaidi ya kata 20 ndani ya Jimbo la Kwela, ambazo ni hekta 67,800. Nimekwenda jana nimezungukia Kote nikakuta Vijana wako wapo site. Nakushukuru Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, ulituahidi Mkandarasi kuanza kazi Scheme ya Ilemba bilioni 21. Tayari tarehe 18 nimekuta anafanya mobilization, nimekwenda nikaongea nae tumekubaliana tarehe 18 Mei,2023 itakuwa ni official launch ya mradi wa scheme ya bilioni 21 pale Ilemba. Hilo Mheshimiwa Waziri, nakushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia kwenye suala la mbolea lakini nataka nizungumzie mambo ya financing model kwenye sekta ya kilimo. Nimeona Waheshimiwa wengi wanaongelea mambo ya Tanzania Agricultural Development Bank lakini ngoja nianze na suala la mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumpongeze Mheshimiwa Rais, kwa kutoa ruzuku kwenye hii sekta ya mbolea, lakini mbolea ilikuwa na changamoto kubwa sana hii mbolea ya ruzuku. Nadhani ni kwa sababu ya maandalizi yalikuwa hafifu. Kwenye Mkoa wetu wa Rukwa, kwanza registration tu wakulima ili waweze ku–qualify kupewe mbolea ya ruzuku, ulikuwa ni mchakato wenye shida kubwa sana. Ulichukua muda mrefu na ilifanyika mwisho mwezi wa 11 mvua zimeanza kunyesha na wakala, kwa mfano ndani ya Jimbo langu la Kwela, tulikuwa na wakala mmoja tu wa ku–supply mbolea kwa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito, sasa tuko mapema tunakwenda kukupitishia bajeti yako, naomba ufanye approval na kufanya vetting ya mawakala walau karibia kila kata. Kata zangu ziko 21 tuwe na wakala wakuwa–supply wakulima mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo muhimu sana Mheshimiwa Bashe. La sivyo, jimbo langu liko so controversial, wewe unalijua umezunguka kule bondeni, kufika Makao Makuu ya Halmashauri Lahela unasafiri zaidi ya kilomita 250. Kwa hiyo, huyu mkulima kwenda kufuata mbolea Lahela, inamgharimu zaidi ya 70,000 na kuendelea. Kwa hiyo, nikuombe tuweke center kila kata ndani ya Jimbo la Kwela, ili wananchi waweze kupata mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia suala la mbegu, kuna mbegu ambazo zimekuwa user friend kwa wakulima ndani ya jimbo langu. Kwa mfano; zao la mahindi tumekuwa tunalima Seed Co 647, Chapa Tembo na Pannar 715 ndio mbegu ambazo wakulima wamezizoea. Sisi TOSC ambao wana certify mbegu hawajatoa kibali kwenye hizi mbegu. Kwa hiyo, wakulima wamekuwa wakitegemea kutoka Zambia. Hiyo sasa imepelekea kuwe na magendo. Smuggling ni kubwa kwenye mipaka, tunachukua mbegu hiyo Zambia na baade tunanufaisha nchi jirani wakati ni jambo dogo sio rocket science.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbegu ambazo tunajua zinawafaa wakulima tunategema nchi jirani. Kwa kweli Mheshimiwa Bashe, kwa umakini wako hii hapana ni aibu kubwa sana. Nikuombe sana hili lifanyie research hizi mbegu zinazokubali za mahindi, zinazotoa uzalishaji mkubwa wa mazao tukazifanyie utafiti, TOSC isiwe na ukiritimba i–certify hizo mbegu wakulima waweze kuwa–supplied mbegu ndani ya Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la mikopo na hiyo ndio Financing mode ya sekta ya kilimo ndani ya nchi hii ina changamoto kubwa. Nakubaliana, kwenye Mkoa wa Rukwa, wakulima walikwenda kuomba mikopo kwenye benki CRDB, NMB na benki zote hizi, walipofika pale wao walitoa masharti kwamba tunakopesha zao la ngano, mahindi hatukopeshi. Hata hivyo, nakubalaiana nao na sababu yao kubwa ni kwamba flexibility yaani sera zetu zimekuwa zikiyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii wakulima wa alizeti walikuwa wanakopesheka kwa miaka minne mitano iliyopita lakini leo hii hakuna benki itakayotoa mkopo kwenye zao la alizeti kwa sababu limeanguka, haliwezi kulipa. Kwa hiyo, benki zimekuwa ziki–divert, zinakuwa zina-hesitate kutoa mikopo kwenye mazao haya. Mahindi wana–hesitate, miaka minne nyuma ilikuwa zao la mahindi halitabiriki. kwa hiyo, mkulima wa mahindi hakopesheki. Serikali mnaisaidiaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wameongelea Benki ya kilimo iwe na tawi kila Mkoa, ile kwanza sio commercial bank, ni development bank ambayo kwa nature ya benki ilivyo sio ya kuwa na tawi kila Mkoa, wilaya wala kila kata. Ni benki ambayo inatakiwa ifanye kazi na mawakala na hilo mmelifanya. Benki ya Kilimo inafanya kazi na CRDB, NMB, TCB shida ni kwamba benki iko undercapitalized. Ina mtaji wa bilioni 267 kwenda 300 lakini mtaji unaohitajika ni trilioni moja. Sasa, trilioni moja mna deficit ya bilioni 700. Pia, Waziri wa Fedha uko hapa, pelekeni bilioni 700 halafu mpeleke kwenye hizi commercial bank ambazo ni mawakala wetu ili wakopeshe wakulima. Hatuhitaji kuwa na physical buildings za mabenki kwenye kila kata ama kila wilaya, tunahitaji fedha zipelekwe wakulima wapate mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha, tunajua kwamba mna–hesitate kuwapa fedha kwenye mfuko mkubwa wa hazina, sawa tuna vipaumbele vingi, basi wapeni approval. Kuna financing kwenye multination financial institution kama World Bank, African Development Bank, BADEA, wako ladhi kukopesha benki zetu ku–boost mitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazuia kwa sababu tunasema tunakwenda kukuza deni la Taifa. Basi deni la Taifa likue kwenye kukuza kilimo kwa sababu hizi hela zinaenda ku–boost kilimo. Kwa hiyo, Waziri wa Fedha na Waziri wa Kilimo, hili jambo ni la kwenu nendeni mkai–boost Tanzania Agricultural Development Bank la sivyo Waheshimiwa Wabunge, mtapiga kele miaka mingi. Kwa mtaji wa bilioni 268 namshukuru Mama Samia, aliyoongeza kwa miaka mingi benki ilikuwa haipewi mtaji. Kwa hili tumpongeze Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa jinsi tunavyokwenda, portfolio ile unaijua Mheshimiwa Bashe, ni ya wakulima wakubwa wachache Bagamoyo Sugar na wachache hawafiki 20 portfolio yote ya Benki ya Kilimo imekwisha. Mkulima mdogo kamwe hatokuja ku–access mkopo wowote kwenye benki yetu ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sasa twende kama tumedhamiria. Haiwezekani uende Tume ya umwagiliaji ukachukua financing moja kwa moja. Kwa nini usipitishie kwenye benki ya Kilimo halafu ili tuweze kukuza balance sheet ya benki ile iweze kukopesheka na mabenki makubwa ya kimataifa na tuikuze iwe ni benki ambayo ni potential itakayokuza sekta ya kilimo ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe nakwambia na haya yote unayajua ndio maana tumesema kwa uwazi na Waziri wa Fedha yupo humu ndani na wewe umo, msaidieni Waziri tukai–boost ile benki, ikifanya vizuri wala hatuhitaji kuwa na physical branches. Wakala tu wa benki kama CRDB, TCB, NMB wana ma–branch nchi nzima. Wanahitaji window zile zifanye kazi isiwe tu ni mapambo ambayo tunawambia wakulima benki ya kilimo, model hivi, no, no. Twendeni tukawe serious, tukakuze kilimo cha Watanzania ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ili na mimi niwe kati ya wachangiaji kwenye bajeti hii ya Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa natoa pongezi zangu za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya. Na kipekee nimpongeze hasa kwa kuijali Wizara hii ambayo kufikia mei 15 alikuwa maewapatia asilimia 84.2 ya bajeti yote tuliyowapitishia mwaka jana, ambayo ni bilioni 175; lakini pia kwa namna ambavyo mwaka jana alifuta malimbukizo ya riba ya pango kwa ajili ya wale wadaiwa sugu. Kwa hili amewasaidia sana Mheshimiwa Waziri kusafisha dawati lenu ili sasa mnapoanza kusimamia jambo la makusanyo ya kodi muweze kwenda vizuri kwa kuwa yale madeni sugu Mheshimiwa Rais amewarahisishia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze kwa bajeti yenu yenye mwelekeo mzuri, wewe Mheshimiwa Waziri na Naibu wako, na tunawatakia kheri, tutakapo wapitishia mkatende yale ambayo mmeyasema kwenye bajeti yenu. Lakini pia nimpongeze Kamishna wa Ardhi Mkoa wa Rukwa, dada yangu Rehema, anafanya kazi nzuri. Kwa muda mfupi ananipa ushirikiano mzuri na Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Rukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nina mambo mawili muhimu. Jambo la kwanza nitaongelea migogoro ya ardhi, na nitazungumzia specifically migogoro iliyopo ndani ya Jimbo langu la Kwera na pengine Mkoa wa Rukwa kwa ujumla. Mwaka jana katika bajeti hii tarehe 25 mei, nilisimama tena kwa uchungu mkubwa na nikaongea maneno makali sana juu ya mgogoro wa ardhi uliopo ndani ya Jimbo langu la Kwera, kwa maana ya mgogoro wa shamba lile la Malonje la Efatha. Lakini Mheshimiwa Waziri mama yangu, dada yangu, rafiki yangu jambo niliona mmelichukulia very lightly. Hamku-take very serious note kwa jambo lile kwa sababu hivi ninavyoongea hatujakaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si kwamba mimi napinga uwekezaji wala nina shida na mwekezaji, Hapana; lakini lazima tufike mwekezaji anapofanya kazi yeye afanye shughuli zake za uwekezaji kwa amani na wananchi wawe na amani. Sasa iliyopo jimboni kwangu ni shida kubwa, migogoro haiishi. Juzi nilikuepo jimboni wananchi wameandamana kwenye Ofisi za chama. Kwa sababu mwekezaji amewaandikia barua kwamba mashamba yote yale waliyolima mahindi hawatakiwi kuvuna mpaka waende kwake yeye. Wakati wamepanda wamepalilia wameweka mbole, wakati wa kuvuna umefika ndipo sasa mwekezaji anakwenda wakamlipe fedha. Na shida ni kwamba ninyi wenyewe Serikali kupitia hii Ofisi ya Ardhi mlileta confusion. Vijiji vilikuwa na mipaka yao na hati yao, kabisa, mkaja kumpa Mwekezaji sehemu ya vijiji, na wanakijiji wana sehemu ileile ya kwao. Kwa hiyo kuna mgongano hapa. Wanakijiji wanadai eneo hili ni la kwetu na mwekezaji anasema hili ni la kwangu kihalali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mgogoro unaenda miaka 13 dada yangu Mheshimiwa Waziri na mwishowe tunaonekana sasa kama wananchi ni wakorofi, wanatumia nguvu nyingi ya dola kuwapiga, kuwaumiza, issue sio kupiga mnaweza mkapiga sasa mgogoro huu ni vijiji 11. Kwangu kwenye Jimbo langu la Kwela ni vijiji vitatu kule kwa ndugu yangu Aeshi vijiji saba, vyote hivi kila muda wapo kwenye movement, maisha yao ya movement.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nikashauri kwamba Waziri aunde tume tuje tukae, tumalize mgogoro, imetosha sasa mambo ya kufukuzana, mwekezaji na pia nilishauri hapa Bungeni, sisi uwekezaji tunaupenda, lakini namna ya shamba lile kuwa idle ekari 23,000 kwenda 25,000 hakuna shughuli inayoendelea, mwekezaji amelihodhi liko idle na pengine kwa sababu ya migogoro pia anaweza kuwa naye hataki kuendeleza chochote. Sasa Serikali position yao ni nini kwenye jambo hili, sisi pale ngano ndio wanaongea, kila siku Waziri Mheshimiwa Bashe naye nilimwambia, anapiga kelele suala la ngano kuna vitu vingine Serikali tumeshindwa tu kufanya maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shamba la hekta 25,000 la mwekezaji wa Shamba la Malonje Efatha liko arable. Tukiwekeza tu pale tutapata tani 175,000 mpaka tani 100,000 za ngano, Waziri ataenda kupunguza deficit hiyo anayopiga kelele hapa, lakini kama halmashauri sisi tutaenda kukusanya mapato kutokana na huo uzalishaji milioni 600, 700 mpaka bilioni moja, lakini katika jambo hili nashangaa kwa nini tunasitasita, sisi hatuna ugomvi, twendeni tukakae pale mezani, tukaondoe huu ugomvi unaoendelea wa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tu imetokea shida tena ugomvi umehama kwa wananchi umehamia tena kwa mwekezaji na Serikali kwa sababu wale wafanyakazi wamechukua trekta lenye harrow wameenda kulima barabara ya TARURA ya kilometa wakaivuruga tu wakailima vuruga. Kilometa 1.5 wanadaiwa wakatengeneze barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunatakiwa tukaweke standard kwamba wewe ni mwekezaji mipaka yako ni ipi, ulipewa shamba kwa madhumuni yapi, ndani ya muda gani utekeleze nini, wananchi mipaka yenu ni hii moja, mbili, tatu. Tuna-close jambo lile kila mtu anaishi kwa amani, kuliko kila mwaka nisimame Bungeni, nina hansard nilikuwa nasoma hapa, mpaka nasikitika walilichukulia very lightly. Madhara yake yanakuja, watauana, wananchi wataamua kum-sabotage mwekezaji na mwekezaji naye anatumia walinzi wake kuwapiga wananchi. Hatuwezi kuuishi kwenye nchi hii kwa namna hii ya kuviziana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri kesho anapohitimisha hili jambo nimeliongea sana, nimwombe alichukulie very serious ili chama nacho kwenye Mkutano Mkuu wa Chama, Mwenyekiti wetu wa Chama Mama Silafu Maufi amesimama pale mbele ya Mheshimiwa Rais akaongelea jambo hili. Kwa hiyo hata Chama kwa Mkoa wa Rukwa wao nao wanapiga kelele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi Mbunge hata Mheshimiwa Aeshi nilikuwa naye hapa, japo yeye anaweza asipate nafasi ya kusema, wananchi wetu wanatutazama juu ya jambo hili. Twende tukakae party zote tulimalize ili tuje na conclusion mwekezaji abaki na amani yake na wananchi wabaki na salama yao ili tukajenge majimbo yetu, yakawe salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili kuna jambo ambalo lipo chini ya mikono ya Wizara, Gereza la Mollo, Gereza la Mollo nalo hivyo hivyo kama alivyokuwa anasema ndugu yangu Mheshimiwa Ndaisaba, wamekuja pale wamewakuta wananchi kijiji kipo wametwaa eneo, wakasema haya tunapitisha mpaka humu tunachukua gereza. Sasa nao huo mgogoro umechukua miaka mingi sasa, inaenda miaka 15, wananchi wanasema ni eneo letu Gereza la Mollo linasema ni eneo letu. Alitumwa wakati ule Mheshimiwa Kangi Lugola akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, akawaambia wananchi tulieni tutarudisha, ikawa ndio jumla mpaka leo. Sasa nawaomba, wao ndiyo waliopewa dhamana ya kusimamia ardhi, waende wakamalize migogoro ya aina hii tusi- entartain migogoro itakuja kusababisha maafa watu wakauana pasipo sababu. Mheshimiwa Rais kama nilivyosema anajali, anawapa bajeti wanaenda huko, waende na mwaka huu hawajaja na waliniahidi watakuja tena alipokuwepo Naibu hapa Ndugu yangu Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete alisema hamna shaka nakuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi kule wanasikia, wanasema mbona Mbunge ulidanganywa. Tumeona pia timu ya Mawaziri Nane kwenye mashamba haya yenye vijiji 11 hawajaja. Nimwombe mama yangu Mheshimiwa Waziri jambo hili mwaka jana aliona niliongea kwa uchungu mkubwa na leo narudia, waje tumalize mgogoro, sisi nasi tunataka tupate mapato kulingana na shamba lile na mwekezaji aendelee na maisha yake, lakini haki ya wananchi itazamwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza jambo la mgogoro, niende jambo la pili la muhimu la kumshukuru tena Mheshimiwa Rais kwa kupandisha hadhi vijiji sita ndani ya jimbo langu kuwa Miji Midogo kwa maana ya Mpui, Kaengesa, Mtowisa, Muze, Ilemba na Kiliamatundu. Sasa vile vijiji vinahitaji kupangiliwa sawa viendane na standard ya kuwa miji midogo. Niombe waisaidie sasa Ofisi ya Ardhi Mkoa kuongeza vifaa vya upimaji, tuna kifaa tu ambacho seti ile ya upimaji pale mkoani tunatumia Kalambo, Nkasi na Sumbawanga DC. Watuongeze ili vijiji vyote hivi ambavyo vimeshakuwa ni miji midogo niliyoitaja waweze kupangilia miji yao na kupangiliwa kwa miji tu hakutakuwa kunaishia hapo, bali kutaingiza mapato ambayo yata-boost mapato ya halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, awali nichukue fursa hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya ya kuwatumikia wananchi wa Tanzania kwa uzalendo mkubwa sana na hasa namna anavyojali na kupeleka fedha nyingi kwenye Wizara ya Nishati.

Pili, nikupongeze wewe Mheshimiwa Spika wa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kugombea nafasi kubwa na nyeti ya kuwa Rais wa Bunge la IPU. Mimi nikuombee heri na mafanikio makubwa kwenye hatua hiyo.

Tatu, nimpongeze sana Waziri wa Nishati Mheshimiwa January Makamba kwa kazi nzuri wanayoifanya akisaidiwa na Naibu wake Mheshimiwa Stephen Byabato, hakika kazi yao ni njema, nami nawatakia heri katika kufanikisha malengo waliyoaminiwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo utajikita kwenye malalamiko au masikitiko yangu makubwa sana juu ya hali ya kusuasua ya utekelezaji wa mradi wa REA Mkoa wa Rukwa. Namba ya Mkataba ni AE/008/2020 -21/HQ/W/31 – LOT 24; Mhandisi Mshauri ni Mercados Aries International; msimamizi ni TANESCO Ltd Mkoa wa Rukwa; Mkandarasi ni M/s JV Pomy and Qwihaya Partnership; muda wa utekelezaji ni miezi 18; gharama za mradi ni shilingi 36,549,180,653.61; wigo wa kazi kwa mkoa mzima.

Mheshimiwa Spika, mradi huu unatekelezwa kwa ushirika wa kampuni ya Pomy na Qwihaya, kwa taarifa za nyuma Qwihaya ni kampuni ya nguzo ila kwa sasa ni mkandarasi wa umeme pia, Pomy ni mkandarasi wa umeme tangu kipindi cha nyuma hadi sasa. Mkandarasi Pomy alishawahipewa kazi ya mradi wa umeme kwa mkoa wa Tabora, alitekeleza mradi huo kwa kiwango kisichokubalika na hakumaliza, lakini adhabu na lawama ilielekezwa kwa wafanyakazi wa TANESCO akiwemo Meneja wa Mkoa.

Mheshimiwa Spika, mwaka uliofuata baada ya kazi ya Tabora kutoisha na kuwa na mgogoro na kukawa na miradi mingine iliandaliwa na REA kwa mikoa mbalimbali ikiwemo Rukwa, sasa wakati wa mchakato huo watumishi wa REA walikataa kumpa nafasi ya kupata mradi mwingine baada ya kuona Tabora kazi iliharibika na maneno ni mengi, hata hivyo alipenya na baadae akapewa mradi kwa Mikoa ya Rukwa na Kagera zikiwa ni lot mbili tofauti. Kwa mkoa wa Kagera vijiji vilivyokwishawashwa umeme ni 36 kati ya vijiji 137 kwa mkoa mzima na kwa mkoa wa Rukwa ni jumla ya vijiji 49 kati ya vijiji 140 kwa kipindi chote hadi mwisho wa mwezi wa nne mwaka huu ikiwa ni miezi minne zaidi ya mkataba wake wa awali.

Mheshimiwa Spika, tangu anaanza mradi huu wa Rukwa kwa kushirikiana na Qwihaya, kumekuwa na migogoro kati yao isiyoisha na kusababisha mradi kutokwenda kwa wakati na kuwa na dalili zote za kutokamilika na huenda mgogoro ukawa ni sawa na kilichotekea Tabora. Tutambue kuwa mradi huu wa Rukwa ulianza kutekelezwa tarehe 9 Julai, 2021 na mwisho wa mradi huu ilikuwa ni tarehe 8 Januari, 2023 na alikuwa amefikia asilimia 38, REA wakaongeza muda wa miezi minne hadi tarehe 30 Aprili, 2023 ili kukamilisha mradi, lakini hadi mwisho wa mwezi wa nne utekelezaji wa mradi ulifikia asilimia 41. Kwa sasa REA wameongeza muda wa kutekeleza mradi huu hadi tarehe 31 Oktoba, 2023.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikifuatilia kwa ukaribu sana juu ya maendeleo ya mradi huu ambao unatupa wakati mgumu sana kwa wapiga kura na nimebaini mambo mengi ya kusikitisha. Pamoja na TANESCO kufanya vikao mbalimbali vya maendeleo ya mradi, lakini hakuna juhudi zozote za makusudi kuhakikisha mradi unakamilika, isipokuwa nilichobaini Mkandarasi Pomy (Eva Fumbuka ambaye ni Mkandarasi Mkuu) kuwa na maneno ya kufajiri bila ya utekelezaji, sababu anazotoa ni kuwa Covid-19 imeathiri upatikanaji wa vifaa, REA hawawalipi na wanaibiwa vifaa site.

Mheshimiwa Spika, TANESCO Rukwa kama msaidizi wa mradi wamekuwa na vikao vya kikazi na mkandarasi kuhusu mradi huu, lakini kwa upande wa mkandarasi mara nyingi wamekuwa wanahudhuria mainjinia tofauti tofauti tena wasio na mikataba ya kazi kwa mujibu wa mkataba wa mradi, kikubwa zaidi ni kuwa Meneja wa Mradi hapatikani eneo la kazi na hata vikao si mhudhuriaji.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuona usumbufu mkubwa sana na kelele ya wananchi kuwa kubwa niliomba mpango kazi na maelezo toka kwa Meneja wa TANESCO Mkoa wa Rukwa ambaye alini-brief kwamba kuna kikao kiliitishwa tarehe 27 Aprili, 2023 kujadili tatizo hilo la Mkoa wa Rukwa na kilifanyika Ofisi ya REA Makao Makuu Dodoma, na Menejimenti ya REA ilikuwa Dar es Salaam hivyo iliwakilishwa katika kikao. Waliohudhuria ni wawakilishi wa Menejimenti ya REA, Mshauri wa Mradi, TANESCO Rukwa na Makao Makuu, Mkurugenzi wa Pomy na Mkurugenzi wa Qwihaya.

Mheshimiwa Spika, katika kikao hicho cha tarehe 27 Aprili, 2023 walijadili changamoto zinazopelekea mradi kusuasua, kama ifuatavyo; mgogoro wa ndani kati ya Mkurugenzi wa Pomy na Mkurugenzi wa Qwihaya katika mambo mbalimbali na kusababisha mgawanyiko wa kiutendaji kama vile suala wa wafanyakazi, usafiri (transport), kugawana vijiji, mvutano wa kufikisha vifaa eneo la kazi, mvutano wa kimaslahi na mvutano wa kimaamuzi.

Mheshimiwa Spika, mgongano wa kimaslahi kwa kuwa mmoja wa Wakurugenzi (Eva Fumbuka) kuwa ni Meneja wa Mradi na kusababisha kuwepo na mgongano wa kimaslahi na wa kimaamuzi, kwenye mkataba kama huu hasa kunapotokea wenye kampuni kutoelewana, Meneja wa Mradi hayupo eneo la kazi ingawa ni mmoja wa Wakurugenzi ni shida mno kupatikana hata kwa njia ya simu, na hashiriki vikao vya kazi kwa mujibu wa mkataba, pamoja na mgawanyiko uliopo wa kiutendaji bado hali ya mradi si nzuri, kubwa zaidi ni kuwa hakuna mawasiliano mazuri kati ya wafanyakazi (wahandisi) wa Pomy na Qwihaya na kupelekea TANESCO pia kuwa na sintofahamu ya mradi.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na hali ya kubadilisha au kuacha kazi kwa wafanyakazi (wahandisi waliochini ya Pomy anaowaweka kama joint venture) bila taarifa yoyote na inapelekea kuharibu mwenendo wa mradi.

Mheshimiwa Spika, baada ya uwasilishaji huo na kuwa na mjadala juu ya hoja hizo, REA walikiri kupokea hoja hizo na kuzifanyia kazi na kwa vile Menejimenti ya REA iko Dar es Salaam basi watawasilisha na kuandaa ripoti ya kikao kwa yale tuliyoyajadili, lakini mpaka leo hii ni mwezi umepita hatuoni chochote kinachoendelea kwani mkandarasi alikuwa kafikia asilimia 41 ya ukamilishaji wa mradi na alikuwa ameomba haraka haraka kwa sababu ya kikao hicho nyongeza ya muda hadi mwisho wa mwezi wa nane, lakini REA kwa sasa wameshatoa nyongeza ya muda hadi tarehe 31 Oktoba, 2023 hii ikiwa ni pamoja na kuongezewa kazi zaidi, nyongeza ya kazi ya kilometa mbili kwa kila kijiji.

Mheshimiwa Spika, jambo la kumuongezea huyo mkandarasi muda (extension of time) kila wakati pamoja na ukweli wote huo wa kusuasua na usumbufu huo wote bado linatupatia jeraha kubwa Wabunge wa Mkoa wa Rukwa. Binafsi sikuona sababu tena za kumuongezea mkandarasi wa aina hii kilometa mbili nyingine kwa kila kijiji kwani ni msumbufu sana na uwezo wake ni mdogo sana.

Mheshimiwa Spika, naomba nihitimishe kwa kumshauri Mheshimiwa Waziri ambaye pia nitamuomba aje Rukwa kwa mara nyingine kujione hali hii. Kwa kifupi mkandarasi Pomy amekuwa ni tatizo kubwa kutekeleza mradi na ni dhahiri kuwa muda wa mradi utaisha hata hiyo Oktoba, 2023 aliyopewa na kazi haitakuwa imekamilika.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri awaagize REA kuupitia mkataba wa mradi na kuona mapungufu yaliyopo na kufanya mabadiko stahiki kwa kuangalia matakwa ya kimkataba, lakini uwepo na utoshelezi wa timu iliyoko Rukwa na Kagera na yote yanayohitajika, kuwataka Wakurugenzi waajiri Meneja wa Mradi kwa upande wa Rukwa na Kagera kama mkataba unavyotaka, ikiwezekana na kwa vile Qwihaya amekwishaona ni tatizo na anachafuliwa na Pomy na anajutia kuingia kwenye hii joint venture na Pomy na kwa sasa kulazimika kuwa na timu yake na kutekeleza mradi, basi timu ya Qwihaya itekeleze mradi kwa Mkoa wa Rukwa na timu ya Pomy itekeleze mradi kwa Mkoa wa Kagera, kuliko ilivyo sasa maana wanalaumiana pia kuwa mmoja anamchelewesha mwingine kuendelea na mradi kwa sababu fulani hajakamilisha kipande fulani.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja na nawasilisha, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii niwe mchangiaji jioni ya leo, kwenye hotuba muhimu sana ya bajeti hii ya maliasili na utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo amekuwa akiijali sana Wizara hii na namna ambavyo anapambana kukuza utalii, lakini upambanaji wake umejidhihirisha wazi kupambana na migogoro na sisi ni mashahidi anaendelea na ndio maana amemuweka waziri makini ambaye kila mtu aliyesimama hapa anaamini matumaini makubwa tunyao juu yako, juu ya utatuzi wa migogoro inayoendelea sehemu mbalimbali hapa nchini. Nikupongeze pia msaidizi wako Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa wizara kwa namna ambavyo mnafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nina mambo mawili; la kwanza, nitaelezea jambo la muhimu sana la kiuchumi linaloendelea ndani ya bonde la Ziwa Rukwa. Mnamo mwaka 2019 Serikali kupitia Wizara ya Madini ilitoa kibali cha Kampuni ya Noble Helium kuja kufanya utafiti ndani ya bonde la Ziwa Rukwa. Bonde la Ziwa Rukwa linahusisha Mkoa wa Rukwa wenyewe, sehemu Katavi na Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wamekuja na wameanza kazi yao tangia 2019, 2020, 2021 na 2022 na utafiti wanaoendelea nao umekuja na matumaini makubwa na sasa kwa utafiti tu wa awali inaonekana kwamba, Tanzania sasa ni nchi ya tatu duniani kwa deposit ya helium ambayo ni gesi adimu, ni critical material ambayo inatumika sehemu nyingi kama mnavyojua siwezi kutaja, kuna sehemu nyingi ambayo gesi ya helium ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni moja kati ya gesi ghali ambayo inauhitaji mkubwa duniani kwa hiyo sisi kama Tanzania kupitia bonde la Ziwa Rukwa, tumepata bahati kubwa ya kuwa na deposit kubwa na wanasema kwamba helium iliyo ndani ya bonde la Ziwa Rukwa ni green helium, ni pure kuliko yoyote ile inayopatikana duniani sehemu yoyote. Ukienda Marekani amabo wanaongoza na ukienda Qatar ambayo ni wa pili na sasa Tanzania tutakuwa wa tatu. Best helium inapatikana ndani ya bonde la Ziwa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika eneo walilopewa kufanya utafiti takribani kilomita za mraba 1467. Kilomita za mraba 167 ziko kwenye hifadhi na hifadhi hiyo ni ndani ya Ziwa Rukwa ambalo Ziwa Rukwa kwa ukubwa wake 80% inamilikiwa na Rukwa - Likwati na Uwanda Game Reserve, zote hizo zinamiliki maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa walianza initiative ya kuomba kibali ili waruhusiwe Kwenda kufanya utafiti maeneo hayo, lakini mzunguko waliopewa zaidi ya miaka miwili, kunaenda nenda rudi. Waliambiwa mara ya kwanza wafanye environmental impact assessment, waka-engage hiyo process, wakatoa taarifa yao, wakapeleka taarifa NEMC. NEMC inka–certify kwamba hamna madhara yoyote na shughuli yenyewe inafanyika ndani ya mwezi mmoja. Baadaye walivyorudisha kwako huko TAWA wakasema hapana, nendeni tena Wizara ya Madini ndio watuandikie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameenda Wizara ya Madini basi kumekuwa na kurushiana mipira mingi. Sisi pale tunaenda kupata faida kubwa, tunaenda kuongeza pato la Taifa, tunaenda kupata kipato ambacho installation ikishakamlika tunaenda kuingiza dola milioni 100 kila mwaka, tunaenda kuongeza ajira na mambo mengi yanaambatana na uvumbuzi wa gesi hii ya helium. Sasa huyu mtu ame-invest zaidi ya dola za kimarekani milioni 30. Anapewa mizunguko hiyo na sasa hivi amekodi vifaa vikubwa ambavyo vinagharimu kila mwezi wanalipa zaidi ya dola za kimarekani milioni 100.5. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vifaa vya airborne survey anavyo pale site kule Rukwa, lakini sababu tu ya kufanya maamuzi. Nakuamini ndugu yangu Mheshimiwa Mchengerwa kamalize jambo hilo wamalize utafiti suala la drilling litakuja baadaye. Tuta–discuss tuone je, kuendelea kuwa na reserve hizi au tuamue ku-drill tuingize mabilioni ya fedha, utakuwa uwamuzi wa Serikali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliongea na waziri wa madini Mheshimiwa Doto Biteko na wewe sasa nakuletea rasmi katika mchango wangu, angalieni mkae pamoja hawa watu wanaingia hasara kila mwezi kupoteza dola za kimarekani zaidi ya milioni moja kusubiria maamuzi ya Serikali ni kuwapa frustration wawekezaji wataona kwamba hatuko serious watanzania kwa jambo nyeti kama hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba niliseme kwa namna hiyo, naamini huyu ni msikivu ndani ya muda mfupi tutamaliza, hawa watu tutawa-sort waendelee na kazi yao ya utafiti na baadaye ripoti watatupa kama Serikali tufanye maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo nije na jambo la pili la muhimu ni migogoro inayoendelea na imesemwa na Waheshimiwa Wabunge wengi. Hapa nianze kwanza tena kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna alivyoridhia maeneo mengi ya hifadhi na kwangu mimi nilikuwa na mgogoro mkubwa sana pale Uwanda Game Reserve kwenye kata ya Kilangarani, Kata ya Kitete pale Kata ya Kapenta na Nankanga tayari maeneo yale yalirudishwa kwa wananchi. Kumebakia Kijiji kimoja ambacho tuna mgogoro Kijiji cha Nsanga ambapo mipaka haikueleweka kulikuwa na mvutano kati ya wanakijiji wa Nsanga na wale wataalamu mliotuma kwenda kuweka demarcation ya mipaka, hawajaelewana.

Mheshimiwa Mwenyekiti naomba hili ni jambo dogo tukali-sort hili suala la mipaka na migogoro ya mipaka tuimalize kwa style hii kwenye hifadhi ya Uwanda Game Reserve. Lakini baada ya pale sasa vioja ndio vilianza na hapa naamini kwamba askari wetu wa hifadhi wengi, wale wasiokuwa waadilifu walitamani migogoro ile iendelee kwa sababu wanaonekana ni beneficiary wa migogoro ile. Nasema hivyo kwa sababu nitaanza mwezi wa pili, jambo hili tumelimaliza Desemba Mwaka jana, mwezi wa pili tu fujo zikaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mweneo yale ambayo Mawaziri walipita wakawapa wananchi, askari tabia zao wanaenda wanamvamia mwananchi wanaswaga ng’ombe wanaingiza kwenye hifadhi. Sasa mwananchi mmoja pale Nankanga anaitwa Nasuminzi ali-resist, alivyo–resist, askari wakaamua watumie nguvu kubwa wakamtandika risasi mguuni na baadaye nilitaarifiwa mwezi ule wa pili, nikawaambia nendeni polisi mkaripoti na ng’ombe wakawa wamenyang’anya. Baadaye iulivyofika ile issue kule polisi, tukaendelea na mazungumzo, baadaye busara ikatumika ikabidi wakae waelewane, yakaisha yule mwananchi akapewa ng’ombe, wakasema tutamsaidia matibabu, mpaka leo waliahidi watamtibu hawajafanya hivyo kwa masikitiko makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamempiga risasi kwa kuswaga ng’ombe wenyewe mle ndani na mimi nililetewa na tumeshirikishana na vyombo vyote vya usalama kuona namna ya ku–handle hii situation na sisi tumegeuka kuwa Wizara kwa namna fulani ku–suppress baadhi ya mambo ambayo tunaweza tukamaliza katika level zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haijaishia hapo kuna mzee mmoja alikuwa na baiskeli anatembea tu, wakamkuta wakasema bwana wewe unasenya kuni humu ndani wakamtandika viboko, wakamchana chana mgongoni nalo hilo tukataka tena kuli-solve wakampa tu shilingi 200,000 za kwenda kufanya matibabu. Nikadhani labda kwa mambo haya kwa sababu tuna-resolve haya mambo katika level ya chini tutayamaliza, naona wenzangu hawaelewi sisi ni wawakilishi wa wananchi na siwezi kukubali kuona mwananchi anaumia nikaka kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 26 Mei, kuna mambo mengine ya hovyo yametokea kule. Wameenda pale tena wanavizia hawa watoto wadogo wadogo, askari wanaenda na gari tena kutumia magari yetu ya Serikali, mafuta yetu, silaha zetu, wakaswaga ng’ombe kule ndani ya hifadhi. Walivyoswaga ng’ombe wakakamata wale ng’ombe wakasema sasa mtalipa. Wale wananchi nina orodha hapa na namba zao za simu nitakukabidhi Mheshimiwa Waziri ili tuanze na mambo haya yanayotuchafua na yanamchafua Mheshimiwa Rais. Wamelipa pale 26,920,000 na hizi hazina control number, wala hazina risiti. Watu wamechukua wameweka mfukoni na ndio maana nimesema kuna watu wanafurahia hii migogoro kwa sababu inawanufaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ndani ya tukio la doria moja tu mnaingiza 26,920,000 kuna utajiri wa namna hiyo? Doria moja ya usiku mmoja. Hawajaishia hapo! Risiti hawajatoa, wameenda wananchi sasa hivi wanavuna, wiki iliyopita nilitengeneza timu yangu kama Mbunge ofisi yangu, nikajihakikishia haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameenda kule site wamekuta wananchi wameanzisha task force nyingine ya kuwanyang’anya mipunga, meeneo yale yale tuliyokubaliana walime. Walilima mwezi wa kumi na mbili na mimi ndiyo nilienda kuwatuliza wananchi kwamba limeni tu tayari na Mheshimiwa Rais kaweka sawa. Wamelima wanawaona, wamepalilia wamewaona, wameanza kuvuna wiki iliyopita wanataka mpunga tena wanachukua wanamnyang’anya mwananchi hapa mpunga, wanauza hapa anaona na hela wanatia mfukoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnadhani kutakuwa na amani Mheshimiwa Mchengerwa? naomba pale utume timu maana yake na sisi tunajipanga kama hamtachukua hatua tutajua namna yaku-deal na wale watu. Hatuwezi kukubali dhuluma, Serikali yetu hii haipendi dhuluma, wala hamkumtuma mtu akafanye dhuluma na nimekuwa nikiwa-engage mimi ni mtu mvumilivu sana na mstaarabu sana. Nimewa-engage taratibu twende tuelewane lakini naona hawa wenzangu hawanielewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba tuma timu na uzuri watu wako menejimenti yako yote iko hapa. Ndani ya siku chache wawarudishie watu mpunga wao wote, nina majina hapa na wanajua na hizi hela hizi ambazo hazikukatiwa risiti 26,920,000 tujue zimeenda wapi? Nani amechukua? Na amechukua kwa sababu gani? La sivyo mzee! Nakuamini kabisa lakini nataka nisite baadaye jumatatu kushika shilingi, lakini naamini jambo hili weekend hii tutalimaliza likae salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninakushuluru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia mawazo yangu kwenye wizara hii muhimu ya Ofisi ya Rais TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu na Manaibu wake pamoja na Katibu Mkuu na timu yake, niwapongeze hakika ni timu ya wachapakazi. Katika mchango wangu wa kwanza nitaongelea mfumo wa ukusanyaji mapato wa kielekroniki, kwa maana ya Local Government Revenue Correction Information system kwa ku-link na pos machines, ni mfumo ambao Serikali ilianzisha kwa nia njema ili kukuza mapato kwenye halmashauri zetu mwaka 2016. Umeenda kwenye processes mbalimbali ya kuziimarisha lakini bado naona kuna changamoto kubwa na gap ninayoiona kwenye huu mfumo ni namna ya ku-entertain collection ya physical cash.

Mheshimiwa Spika, dunia ya leo imeenda mbali sana, mambo ya physical cash yamepitwa na wakati, lazima tutafute namna mfumo huu utakuwa friendly tuanze kukusanya mapato yetu kwa kutumia soft money, na hii ndiyo maana unaona katika ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, halmashauri zetu walikusanya zaidi ya bilioni 18 na hazikwenda benki. Sasa kwa sababu ya ku-entertain cash, ndiyo maana unakuta bilioni 18 haziendi benki.

Mheshimiwa Spika, sasa nikushauri Mheshimiwa Waziri, kama itawapendeza, nendeni mkaupitie huu mfumo kwa undani zaidi, kwasababu umekuwa na loop holes nyingi. Mfano, anayeshika hii pos machine ni mtaalamu wa TEHAMA na huyo anauwezo wa ku-delete transaction, anapigiwa simu anaambiwa bwana hiyo haikuwa laki tano ilikuwa elfu tano na hii imepelekea kwenye Hesabu za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, bilioni nne zilifutwa. Sasa hizi bilioni nne zingeweza kufanya vitu vingapi kwa kuleta maendeleo kwa Watanzania!

Mheshimiwa Spika, na nionge with very serious note, kwenye halmashauri yangu zaidi ya milioni 400 zilitoka huko nje mpaka leo tunavutana na tunakaa tunang’ang’ana tuwapeleke polisi, tuwafunge tutawamaliza watendaji woote, wa kata na wa vijiji na wote wanaoshika pos machine, bila kuja na solution ya kuondoa physical cash tukawa na ile ambayo ni soft cash, tutawamaliza na hii defaulters itafutika, itakuwa historia tena mwaka huu mki-test, mtaona na kama mnataka muone cash management solution, nendeni kwenye benki watakupa, ni gharama ndogo tuna vijana wetu waliosomea IT watatupa ujuzi huu ni namna gani tunaweza kufanya cash management solution kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa spika, kwa hiyo, nikuombe with due respect Mheshimiwa Waziri, nendeni mkaone namna ya kufanya jambo hili ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia mchango wangu wa pili, naomba kuongelea mahusiano kati Wakurugenzi wa halmashauri, Madiwani na Wabunge.

Mheshimiwa Spika, nitaanza msemo mmoja kwa ruhusa yako ya kilatini, unasema Helius Beneficum cum servire regnire est maana yake ni kwamba, ni jambo jema sana na lenye baraka kuchagua wale ambao unawatumikia ni kutawala pamoja nao. Sisi wanasiasa tulivyoenda kuomba kura kwa wananchi wakiwepo Waheshimiwa Madiwani, Waheshimiwa Wabunge, tulichagua kuwatumikia, ambao kuwatumikia ni kutawala pamoja nao, lakini kuna baadhi ya halmashauri huu msemo umekuwa ni tofauti kabisa, na nitolee mfano wa halmashauri yangu.

Mheshimiwa Spika, nimebahatika kuhudhuria vikao vya finance mara mbili, nimekutana na mambo ya ajabu kabisa! Inafikia Mkurugenzi anasimama na kuwatukana Waheshimiwa Madiwani, anamtukana Mbunge, anaitukana Kamati za Hesabu za Serikali LAAC kwamba hawezi kumfanya kitu chochote, ameteuliwa na Rais, hii dharau ni ya kiwango cha juu haiwezi kuvumilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na leo hii ninavyoongea Madiwani wangu walikuwa na kikao cha baraza la Madiwani wiki hii, Mkurugenzi kwa kujisikia tu akawaita anavyotaka, wao wameenda pale wanasubiri na hivi Kamati ya Usalama na Ulinzi iko pale kesho atafanya kikao, aje asije huko ndiyo tulikoenda.

Nikuombe sana Mheshimiwa Ummy ili uweze kutusaidia sisi hasa wananchi wa Jimbo la Kwela walituchaguwa wanataka wakaone tunavyo-deliver, tunavyowaletea maendeleo, hatuwezi kuwa na halmashauri ambayo ina mgogoro, Mkurugenzi ana kiburi, kama anafikia hatua ya kuweza kumtukana Mkuu wa Mkoa, anamtukana RC, anamtukana Mkuu wa Wilaya, kuna maisha hapo tena!

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, halmashauri imebaki kama kijiwe tu pale, na nikuombe, fedha ambazo umepeleka juzi, nililikufua sana mkatupelekea bilioni 2.5, kazifuatilieni fedha hizi za mradi kwa sababu pale kumebaki kama kijiweni with very serious note. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi sikuongea kwa hiyo, nilimwambia, mimi ninaenda kwenye platform yangu Bungeni nikaeleze na Tanzania nzima isikie, kwamba sitaki mchezo, wanananchi walinichaguwa na hili nimekuomba mama, tutakutana tena kwenye shilingi ya mshahara wako, ili nihakikishe limefanyiwa kazi, halmashauri yangu imerudi kati ya halmashauri ambazo zinaheshimika na Waheshimiwa Madiwani wapewe heshima yao. Hivi kweli mtu unaitukana Kamati ya Bunge, kwamba mimi niliteuliwa na Rais, mtu anayeweza kunioji ni Rais tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ninaomba kwa kweli tuangalie hata Walaka wa Mwaka 2011, mliwapa pawa sana wakurugenzi wakabaki kwenye loop hole ya ku-hang, mwishowe wanaanza matusi, kunidharau Mbunge, kumdharau Diwani, umedharau wananchi. Kwa hiyo, nikuombe sana, nimeongea kwa uchungu mkubwa, nadhani ndugu yangu Silinde wewe classmate wangu umenielewa, nimekueleza mara nyingi, Mkuu wa Mkoa ameleta barua nyingi RC, kumekaa kimya, nendeni mkainusuru Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu pia kuongelea jambo la TARURA, TARURA wameongea, sihami sana kwenye concept yao, twendeni tuka-review mgawanyo wa fedha hizi, huu mgawanyo umekuwa unfair! Baadhi ya halmashauri zina kilometa chache zinapewa triple au twice kuliko halmashauri zenye network kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu ni kuumiza wengine, kuna baadhi ya kata tangia watoe, halmashauri iache kuudumia barabara, wana maisha magumu, hawajawahi kuona hata greda. Nina Kata kama Mnangalua, Kata ya Mnokola, Kata ya Nankanga, Kata ya Kalambanzite, Kata ya Kaengesa, Kata ya Kanda, ninaweza nikazitaja kata hapa, wanalia, naombeni nendeni mka-review upya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuongeza fedha TARURA ni jambo la kwanza, lakini jambo la pili, wajitahidi kuhakikisha mgawanyo unakuwa fair kwa kila halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe pia nichangie kuhusu huduma ya afya, na hii ndugu yangu Silinde utakuwa unamnong’oneza hapo Mheshimiwa Waziri. Wewe tunatokea jirani pale na Tarafa yangu ya Kipeta ni jirani pale na wewe, ile Tarafa tangia uhuru haina kituo cha afya na ina wakazi wanakaribia laki moja, wala haina miundombinu yoyote ya maji, wao wako kama wapo jangwani, ni kama wana ambao wametelekezwa. Nikuombe sana, wamekuwa wakija pale Kamsamba napo huduma zinaenda kwa kusua sua kwa ndugu yangu Conchesta pale.

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana, angalieni namna tutaanza kuisaidia hii Tarafa ya Kipeta, ipate kituo cha afya kwa haraka. Kwasababu maisha ya wananchi hawa ni hatari, juzi watu walikuwa wanakwenda pale kijijini kwenu Mkulwe, wameliwa wananchi 15 wamedumbukia kwenye mto, tumeishia kuzika wananchi wanafuata huduma ya afya huko ng’ambo. Nikuombe sana ndugu yangu tushirikiane kwa pamoja, tuhaikishe haya mambo yanaenda ili kuweza kuleta ufanisi ndani ya halmashauri yangu na Taifa la Tanzania kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na hayo tu, niwaombe sana mkayafanyie kazi, hakika wananchi wangu wa Jimbo la Kwela na Waheshimiwa Madiwani wangu wao tu hawalii kilio tu cha stahiki, na kutukanwa matusi juu, na wamerudi nyuma, Mkuu wa Mkoa leo alikuwa ananipigia simu anasema, sasa tutaendaje Mheshimiwa Mbunge, nikasema hapana, wananchi walipanga mstari kutupigia kura, hili jambo lazima Serikali itatusikia na itafanya hatua ya haraka sana.

Mheshimiwa Spika, Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu niliotumwa na wananchi wa Jimbo la Kwela na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla, kuhusu sekta hii muhimu ambayo inagusa maisha ya wananchi wa Mkoa wa Rukwa. Sitakuwa nimewatendea haki wananchi wa Jimbo la Kwela na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla kama sitaongelea hali halisi ya zao la mahindi ndani ya mkoa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini Mheshimiwa Aida amesema hapa na naomba nisisitize kwa umuhimu wake, leo hii inaonekana Mkoa wa Rukwa tumekuwa kama kichwa cha mwendawazimu. Mwaka jana nilipata masikitiko makubwa katika hotuba yake alivyokuwa anahutubia Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI wakati huo Mheshimiwa Jafo, akawa anasema kati ya mikoa ambayo yamechangia na kupata mapato ghafi kidogo sana na ya mwisho katika mikoa yote Tanzania ulikuwa Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sababu kubwa iliyopelekea tukae mkiani, sio kwasababu sisi hatufanyi shughuli, ni wavivu, hatulimi wala hatujielewi, hapana, wananchi wa Mkoa wa Rukwa wanajituma sana, tunalima na sisi ndio katika top two katika kilimo cha mahindi nchi hii, Mkoa wa Rukwa ni mmojawapo. Nimekuwa nikifuatilia sana mijadala hapa Bungeni, mwezi Februari nilisimama katika Bunge hili Tukufu, nikaongelea suala la zao la mahindi, lakini pia kuna Wabunge mbalimbali akiwepo Balozi Dkt. Pindi Chana aliuliza swali katika Wizara hii, lakini majibu ya Naibu Waziri yalikuwa ya kukatisha tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka wakati huo katika Bunge la Kumi na Moja mtu ambaye nilikuwa ninam-rank kama the best of Rukwa Region alikuwa ni Mheshimiwa Naibu Waziri Bashe, alikuwa ni front liner na champion mkubwa wa kupigania zao la mahindi, alikuwa anatoa takwimu unit cost ya production per heka na mauzo anayouza mkulima kwa heka moja. Alikuwa anasema gross loss ilikuwa ni Sh.150,000 kwa mkulima kila msimu. Bahati mbaya wakati huu hiyo gross loss anayopata Mkulima kwa heka moja imeenda mpaka Sh.300,000 yaani unapofika wakati wa mavuno, akijumlisha gharama zake za uzalishaji mkulima wa Mkoa wa Rukwa anapata hasara ya Sh.300,000, hapo hajatunza mazao, afanye hedging asubiri bei itakapopanda, hivi ninavyoongea Sh.18,000 gunia moja, heka moja Sh.700,000…

SPIKA: Mheshimiwa Deus Sangu mimi shahidi yako, nilikuwa nikikaa hapa Mheshimiwa Bashe yupo pale nyuma anashuka jinsi wakulima wa mahindi ambavyo hawatendewi sawasawa kwa hesabu kwa takwimu, sasa leo yupo wapi? (Makofi)

MHE. DEUS C. SANGU: Yuko hapa.

SPIKA: Haya endelea kuchangia Mheshimiwa.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniunga mkono. Kwa hiyo Mheshimiwa Bashe ni msalaba wake huu, is your baby, naomba leo wakiwa wa Waziri hapa Profesa waje watuambie wananchi wa Mkoa wa Rukwa na Nyanda za Juu Kusini, wanawapa habari njema. Habari ya kusema kwamba mipaka ipo wazi, hiyo sio stori brother, lazima waanzishe marketing intelligent system waende kwenye nchi hizo ambao wanadhani ni masoko, mpaka unaweza ukawa wazi, lakini sio wazi kwa Tanzania pekee, Zambia wanaangalia hiyo mipaka iliyo wazi; Kenya wanaangalia mipaka iliyo wazi; DRC wanaangalia mipaka iliyo wazi na Burundi hivyo hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa wakikaa kwenye madawati huko Wizarani wanasubiria tu kwamba mipaka iko wazi you will wait until the next coming of Jesus Christ. Kwa hiyo namwomba sana Mheshimiwa Waziri kwa Mkoa wetu wa Rukwa, leo hii halmashauri zetu zime-paralyze, hazina mapato, sisi hatuna migodi ya dhahabu, hatuna jambo lolote tunalotegemea zaidi ya zao la mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya hadi mpunga sasa umeshuka bei. Mwaka jana hali ilikuwa ngumu. Halmashauri zetu zote katika Mkoa wa Rukwa zimeshindwa kukusanya mapato. Tumeshindwa kujenga madarasa, tumeshindwa kujenga zahanati, tumeshindwa kuboresha vituo vyetu vya afya, maisha ni magumu watuonee huruma wananchi wa Mkoa wa Rukwa, tumechoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna solution zinatolewa kwamba substitute, twende tupeleka mikorosho na wakituletea mikorosho its good initiative, lakini haitoshi, wakileta mikorosho ina maana tuache kulima mahindi. Tukiacha mahindi maana yake nchi itaenda kwenye baa la njaa, baadaye wataanza kuhangaika kutafuta mahindi sehemu nyingine. Kwa hiyo, hatutaki korosho iwe ni replacement ya mahindi, tunataka iwe ni alternative tu, anayetaka ku-jump kwenye korosho ataenda, anayetaka ku-jump kwenye mazao mengine ya kimkakati ataenda, lakini hatutaki mahindi yawe replaced, tunataka mahindi yabaki kuwa pale pale, kwa sababu wakati wa njaa sisi ndio mkombozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi ikiingia kwenye matatizo ya njaa, Wizara inakimbilia Rukwa, sasa hivi mazao tumefanya over production wanaanza kutukimbia wanatukwepa na sababu ndogo ndogo. Nilienda front line, tukaenda mpaka wa Waziri Mkuu tukamwambia huu ni mwezi Februari Mheshimiwa Waziri Mkuu tunaomba na akaja kusema ndani ya Bunge hili Tukufu kwamba tayari tutaunda timu itakayoenda huko Kongo na Burundi ili ku-secure hayo masoko.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwa na dhamira njema na safi, lakini naona watendaji wake hawaendi na sauti ile, ilitakiwa tamko la Waziri Mkuu hapa liwaamshe, waje tukae Wabunge wa Mkoa wa Rukwa na management ya Mkoa wa Rukwa, twende huko, baadaye tutakuta yale masoko yameenda, hatuna soko la mahindi, confidence ya wakulima imepotea, wamekata tamaa.

Mheshimiwa Spika, nawaheshimiwa sana Mheshimiwa Bashe na Mheshimiwa Waziri, sitaki kesho niendeshe mgomo wa Wabunge wa Nyanda za Juu Kusini, tuwawekee mgomo wa Bajeti yao mpaka waje na kauli thabiti, kauli ambayo sasa tukirudi mwezi Julai kwenye ziara kwa wananchi, tuwe tunawaambia jambo linaloeleweka sio stories. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, naomba tu niseme hayo kwa uchache, ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia kutoa mawazo yangu katika Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kufikisha salamu za wananchi wangu wa Jimbo la Kwela. Wamenituma nisimame ndani ya Bunge hili Tukufu nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais kwa mambo makubwa aliyotufanyia. Mwanzoni mwa Bunge hili nilikuja kulalamika, tulikuwa na maafa makubwa; madaraja karibia 18 yaliondoka katika Jimbo langu. Nashukuru Mheshimiwa Rais katika Awamu hii ya Sita ametutizama kwa jicho la huruma, ametuletea fedha takribani shilingi bilioni 3.6 za kwenda kurekebisha madaraja haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi katika barabara ya Kata 13 za Bonde la Ziwa Rukwa, Mheshimiwa Rais ametukumbuka katuletea shilingi bilioni 4.8. Kwa kweli wananchi wamesema tufikishie pongezi kupitia Bunge hili Tukufu ili Mheshimiwa Rais ajue Wana-Kwela wanathamini jinsi anavyowajali na anavyowakumbuka wakati wa matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, isitoshe ametuletea shilingi bilioni moja kujenga ofisi ya Makao Makuu katika Mji Mdogo wa Laela na shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya miradi ya afya na elimu. Wananchi wa Jimbo la Kwela ndani ya kata zote 27 wanampongeza Mheshimiwa Rais, wanamwombea afya njema na siha, aendelee katika speed hii hii aliyoionesha ndani ya miezi hii mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, isitoshe, shilingi milioni 500 ambazo tumetangaziwa neema na Waziri, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, pia shilingi milioni 600 za barabara; na wananchi wa Jimbo la Kwela pia wanamshukuru Mheshimiwa Rais na timu yake ndani ya Serikali kwa namna ambavyo amekuja kwa kasi ya ajabu kuwaletea wananchi maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna shukurani ambazo nimetumwa na Waheshimiwa Madiwani wa Jimbo langu kwamba katufikishie salamu kwa kutukumbuka. Nasi tunaanza kulipwa kutoka kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina. Shukrani ya pekee wanaomba, angalau hii isiishie hapa, iwekewe sheria maalum ili kesho asije mtu mwingine akabadilisha kwamba hii ilikuwa batili. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, nakuletea hii habari ya Madiwani wangu, naomba uisikilize na mkaifanyie kazi, muifanyie reinforcement. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nitoe pongezi kwa Wizara hii ya Fedha. Nakupongeza ndugu yangu, First Class Economist, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwa kweli unaitendea haki hiyo First Class yako ya uchumi. Ndugu yangu kwenye Kamati yangu tulikuwa naye PAC, tulikuwa tunamwita Engineer wa Kamati ya PAC. Kweli kazi mnayoifanya kwenye Wizara hii ya Fedha mna- deserve sifa kubwa sana, mmetuletea bajeti ambayo ni realistic, ambayo inakuwa communicated. Tunai- communicate vizuri kwa wananchi na wameielewa. Naomba kwa spirit mliyokuja nayo mwendelee hivi hivi. Kweli Watanzania wanaanza kupata matumaini makubwa kutokana na bajeti hii ya kwanza katika Awamu hii ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa pongezi zangu, nina mambo ya kuishauri Serikali. Naomba hapa tusikilizane vizuri kwa umakini mkubwa sana. Ni-declare interest kwamba, nisipoona mkulima wangu au wakulima ndani ya nchi hii wanatetewa, nakuwa mnyonge kwa sababu kwanza mimi binafsi ni mtoto wa mkulima. Nimekuja niongelee jambo moja kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, NFRA - Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula, ndiyo instrument pekee ya Serikali ambayo inaweza ikawa na touch au DNA na wakulima wetu kwa sababu hili ndilo soko la uhakika la wakulima kwa mazao yetu ya nafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa napitia bajeti hapa. Tumewatengea bajeti ya shilingi bilioni 14. Mwaka wa fedha uliopita ilikuwa shilingi bilioni 15; kwa hiyo, kila mwaka tunapunguza kidogo. Miaka minne back hapo, tulikuwa tunawatengea shilingi bilioni 100. Sasa tunapoi-cripple hii NFRA maana yake tumeamua tuwazike wakulima wetu na hawa ndio wata-participate vizuri katika ku-implement bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tukafikirie, NFRA ina vyanzo vingi, achana na grant ya Serikali, wao pia walikuwa na room ya kwenda kukopa kwenye Commercial Bank. Mwaka 2019/2020, nina story naisikia kwamba mmewazuia Wizarani kwako Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, fieldmarshal, nasikia hamtoi vibali, wakakope. Wamekopa shilingi bilioni 35, lakini wamerudisha kwa uaminifu mkubwa, mpaka Commercial Bank nyingine wamethamini kwamba NFRA ni wateja wazuri. Hizi hela hawaendi kulipana posho, zinaenda kununua mazao hata kwa dada yangu, Mheshimiwa Jenista Mhagama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana, nendeni mkatoe hicho kibali NFRA wakachukue hizo bilioni nyingi, warudishe kwa wakulima, wanunue mazao; na kwa sababu jukumu lao ni kutafuta masoko nje, wataenda kuuza huko, tutafanya recycling ya ile, itarudi tena kwenye mzunguko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa construction industry imefanya vizuri tume-invest mabilioni ya pesa; na ndiyo inafanya vizuri, ime-contribute asilimia 13 katika uchumi; kilimo 4.8; lakini investment kwenye kilimo ni short term investment ambayo impact yake tunaiona kwa haraka. Msiwanyime, waende kwenye Commercial Bank na ziko willing kutoa hiyo mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba kabisa, ndugu zangu naamini ninyi ni wasikivu, naombeni msikilize ili mkawakomboe wakulima. Kwa sababu mtapopeleka fedha ile tunaongeza purchasing power yao na ndio hao wataweza kuonja kwamba tuko kwenye uchumi wa kati, kwa sababu ya fedha zile tulizowapelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja ambalo limekuwa likisikitisha na hili naomba niongee nikutwishe mzigo dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama. Kutokana na ripoti ya CAG, inaonesha NFRA ilikopwa na Kitengo cha Maafa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, shilingi bilioni 167. Hizi zinanunua karibia tani 365,000. Sasa miaka 12 hamjarudisha hata senti moja, nendeni mkaweke utaratibu mzuri tukawalipe walau kwa installment 12 years, hawarudishiwi kitu chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutai-paralyse hii institution ya NFRA ambayo ni muhimu sana kwa wakulima wetu masikini wakiwemo wakulima wa Mkoa wa Rukwa, Ruvuma, Njombe na Iringa wanaitegemea sana NFRA. Nawaomba mwende kama Wizara, m-discuss jambo hili muone ni namna gani ambayo mtarudisha hizi fedha kwa wakulima. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULAMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULAMAVU: Namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa kukumbusha hilo deni ambalo anasema limejitokeza kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu. Naomba tu kumpa taarifa kwamba deni hilo ni yale mahindi ambayo yanakwenda huko huko kwenye Halmashauri za Waheshimiwa Wabunge ili kushughulikia matatizo mbalimbali wakati wa maafa na vitu vya namna hiyo, lakini hasa wakati wa maafa, ndiyo yale mahindi tunayowaletea huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote, ulizaneni kwenye Halmashauri zenu; Halmashauri ambazo hazijalipa zirudishe hiyo fedha haraka sana ili iweze kufanya hiyo kazi ambayo Mheshimiwa Mbunge anaishauri.

Kwa hiyo, naomba nitoe hiyo taarifa, nadhani Mbunge atakubaliana nami Halmashauri waharakishe kurudisha hizo fedha. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Mbunge unapokea taarifa hiyo nzuri?

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Taarifa hiyo naipokea, lakini mzigo mzigo tunawakabidhi Wanyamwezi kwa maana Ofisi ya Waziri Mkuu watusaidie kulibeba hili. Huko Halmashauri ni wadogo, likiwa kwa mkubwa, Waziri Mkuu naamini litafanyiwa kazi kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo moja. Nchi yetu kama Tanzania tuna advantage kubwa. Kwenye uzalishaji; productionwise na locationwise katika nchi zilizopo kwenye ukanda wa Maziwa Makuu, tuna faida kubwa. Sasa NFRA walishapewa mandate; katika dhima yao mojawapo ni kuhakikisha usalama wa chakula nchini kwa kununua, kuhifadhi na kuzungusha chakula. Kwa hiyo, wanaruhusiwa kufanya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Waziri Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu hapo, tusaidieni, kaiwezesheni hiyo ofisi ika-capitalize hayo masoko yaliyopo katika nchi za Maziwa Makuu ili tukawanusuru wakulima wetu. Kama tukiwa serious kweli kuiwezesha hii NFRA, nawahakikishieni nchi yetu tutaenda vizuri katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuwa mchangiaji wa kwanza jioni ya leo. Katika hoja tatu kubwa zilizowasilishwa jioni ya leo. Hoja ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, Hoja ya Kamati ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma na ile Kamati ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, katika fursa hii niliyopata mimi mjadala wangu utajikita katika taasisi kubwa mbili. Leo nitajadili Fungu Namba 28 – Jeshi la Polisi na Fungu Namba 93 – Jeshi Uhamiaji. Katika ripoti ya CAG na ripoti iliyowasilishwa leo na Kamati ya PAC kuna mambo muhimu ambayo yamezungumzwa; na mimi katika uchambuzi wangu nitaanza na Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Jeshi la Polisi, katika ripoti ya CAG na ripoti ya Kamati imeonesha ndani ya Jeshi la Polisi kuna mfuko ambao ulianzishwa na Jeshi la Polisi unaoitwa Reward and Fine Fund ambao kwa jina lingine unaitwa Tuzo na Tozo. Mfuko huu ulianzishwa kwa nia njema. Nia ya Serikali au Jeshi la Polisi ilikuwa ni kwa ajili ya ustawi wa Polisi ili kuwawekea mazingira mazuri, ikiwemo ujenzi wa nyumba zao na miradi mbalimbali. Lakini uanzishaji wa mfuko huu ulikuwa na sheria yake, na sheria ile ilitungwa; na kulingana kufuatana na taratibu na mahitaji ya sheria ya fedha na kufuatana na kuanzishwa kwa mfuko huu miaka 10 ilitakiwa kwanza ipate idhini, kwa maana kanuni zitungwe na Waziri mwenye mfuko husika.

Mheshimiwa Spika, lakini cha ajabu mpaka hivi ninavyoongea ni zaidi ya miaka kumi na CAG amebaini kwamba mfuko huo umekuwa ukipokea ela na unafanya matumizi lakini Waziri hajawai kutunga kanuni zinazoelekeza namna fedha zitumike. Tafsiri yake ni kwamba mfuko umekuwa ukijiendesha kienyeji.

Mheshimiwa Spika, nataka kusema, kwamba fedha zimekuwa zikikusanywa na chanzo kikubwa cha fedha kwenye mfuko huu ni huduma ambazo wamekuwa wanazitoa kwenye ulinzi wa taasisi za fedha, migodi na sehemu nyingine. Mfuko huo una fedha nyingi na Jeshi la Polisi linaweza kukusanya bilioni 10 hadi bilioni 15 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, lakini fedha hizi hazina mwongozo wa kanuni uliotungwa na Waziri, hakuna Mhasibu wa kusimamia mfuko huu na haujawahi kukaguliwa tangu uanzishwe na CAG, na, hakuna hesabu zilishawahi kufanywa kwenye mfuko huu. Bahati mbaya huu mfuko kuna ukiukaji mkubwa sana. Kwa mfano mkataba unaingia na taasisi ya fedha, let us say wanaingia mkataba wa milioni 80 kwa mwezi; sasa mchezo unaofanyika ni kwamba, wale Askari wanaopangiwa kwenda kufanya majukumu wanalipwa posho kutokana na hizo fedha, na baadaye Jeshi la Polisi likihitaji malipo wanakata kulingana na ile fedha waliolipa kwanza wale Polisi waliotoa huduma.

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kwamba kunafanyika matumizi ya fedha mbichi. Yaani ina maana wanafanya invoice discounting wanachukua ela yao mapema. Hapa pana-create mwanya, fedha zinaweza zikachukuliwa nyingi. Kama Jeshi la Polisi lilitakiwa kukusanya milioni 80 unaweza ukakuta mwisho wa siku invoice wanayo peleka ni milioni 20, milioni 80 zimechukuliwa zikiwa mbichi.

Mheshimiwa Spika, mimi sipingi askari wetu wanapofanya kazi ya kulinda malindo haya kupewa risk allowance, lakini risk allowance lazima iwe na utaratibu wake kwa miongozo ya Sheria ya Fedha. Huwezi ukachukua tu huko benki unakolinda kwamba wanakulipa huko huko. Benki au migodi imeingia mkataba na Jeshi la Polisi, kwa hiyo ilibidi fedha zote ziingie kwanza kwenye mfuko halafu Jeshi la Polisi lifanye arrangement ya kuwalipa askari kule kule na si kule wanapofanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jambo hilo limeendelea na haijulikani sasa utaratibu upi wanafanya ili kufanya reconcialiation ya fedha hizo. Hivyo, Kamati iliona na CAG aliona kupitia mazingira haya kunaweza kukawa na upotevu wa fedha nyingi kwa sababu control yake ni ngumu.

Mheshimiwa Spika, CAG alielekezwa kwenda kufanya ukaguzi maalumu kwenye mfuko huu ambao umekaa zaidi ya miaka kumi haujafunga hata hesabu zake. Mpaka sasa hivi kuna kigugumizi na ushirikiano wanaopata ni mdogo. Sasa nashindwa kuelewa ni kwa nini CAG hapewi ushirikiano wa kufanya hii special audit ili sasa umma ujue na sisi Wabunge kwa niaba ya wananchi tujue, fedha hizo zilizokusanywa kwenye mfuko huo ni kiasi gani, matumizi yake yalikuwa yapi na kwa nini kanuni ya kuongoza na kuguide namna ya matumizi ya mfuko huo hazijatungwa mpaka leo? Sipati majibu ya mambo haya na mabo yanaendelea.

Mheshimiwa Spika, Mfuko huu ni mfuko ambao una fedha nyingi, na umesikia mara nyingi hata Mheshimiwa Waziri akiwa anajibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge, wakiomba kituo cha Polisi anawaambia tutaenda kuchukua kwenye tozo na tuzo. Lakini hiyo, tozo na tuzo haina control yoyote, ni kama kichaka fulani hivi. Sasa hatuwezi katika nchi hii, na hizo fedha hazipitishwi wala haziidhinishwi na Bunge, zinaishia huko. IGP anamwandikia Pay Master General; anataka bilioni 10, zinakuja kwa IGP zinaenda kwenye matumizi moja kwa moja, hakuna utaratibu wa namna hiyo. Hivyo, kuna ukiukwaji wa Sheria ya Fedha maana hakuna control yoyote wala hesabu zinazowekwa.

Mheshimiwa Spika, sasa niombe nishauri mambo yafuatayo; mfuko huu una fedha nyingi, pamoja na kutumika hadi anapoondoka CAG zipo fedha kwenye akaunti yao huko BOT, bilioni 35 karibia na milioni 300 na kidogo, na bado wanaendelea kukusanya. Niombe, kama tuna nia njema na tunataka kuweka transparency kwenye matumizi ya fedha za umma, niombe mambo yafuatayo: -

i. Wa-suspend matumizi kwenye mfuko huu mpaka kanuni ziundwe na Waziri mwenye dhamana.

ii. Serikali ijikite kwenda kumpa CAG ushirikiano afanye audit ili tujue kuna nini na fedha hii imetumikaje kwenye mfuko huu.

iii. Tuombe wakaandae hesabu, inakuwaje mfuko ambao hauna mhasibu upo tu na billions of money zipo tu zinachukuliwa kiholela. Waende pale wakatuandalie hesabu na sisi tuweze kujua ni jambo gani linaendelea kwenye mfuko huu wa tozo na tuzo.

Mheshimiwa Spika, Kuna njia rahisi, tuwasaidie Serikali, tunahangaika tunashida na vituo vya polisi nchi nzima. Tengenezeni arrangemet kwani kile chanzo kina fedha ambazo ni stable and sustainable, nendeni kwenye financial institution mkaombe mortgage mjenge kwa wakati mmoja Vituo vya Polisi nchi nzima. Halafu, kwa kuwa ile fedha kwa kuwa source iliyo stable mtaenda kulipa huo mkopo na tutakuwa na Vituo vya Polisi nchi nzima bila upendeleo na kila mtu ataona manufaa ya mfuko huu, kuliko wakati huu ambapo IGP akiwa huru ataona sasa hivi nina interest na sehemu gani ngoja nikajenge majengo hapa. Akiondoka IGP huyo ana-abandon majengo yale anakuja IGP mwingine anaanzisha uelekeo wake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hatuna direction kwenye mfuko huu. Kama nchi tutafakari kwa pamoja, twende tukafanye jambo la muhimu kwenye mfuko huu, ili uletwe. Na kwa kuanzia mwaka wa fedha ujao tupitishe hapa makadirio ya mapato na matumizi ya mfuko huu ndani ya Bunge hili na hapo ndipo tutakuwa tumefanya kazi. Tumekosea sana tumevunja Sheria ya Fedha, hatujali tunaenda tu.

Mheshimiwa Spika, niombe sana, Serikali ipo hapa, hili jambo mkiendelea ni bomu kubwa sana, kuna ubadhirifu mkubwa upo hidden kwenye huu mfuko. Mkiuacha bila Kwenda kuufanyia hatua za haraka bomu litakuja kulipuka, tusije tukalaumiane.

Mheshimiwa Spika, hilo nimemaliza. Nadhani watakuwa wamenielewa juu ya mfuko huu wa tozo na tuzo. Niwaombe kabisa tena mambo mengine ya kuja kutuambia tutakwenda tutaenda kuchukua; m-suspend huo mfuko mpaka mfuate taratibu zote zinazo wahitaji kama Serikali ili kusiwe na mkanganyiko. Hiyo nimemaliza naomba niende kwenye fungu lingine la uhamiaji Fungu Namba 93.

Mheshimiwa Spika, hii ni taasisi nyingine iliyo ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani. Mambo ya kusikitisha kabisa, nitatoa literature moja juu ya kilichotokea pale Uhamiaji. Alisema hapa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, kuna habari ya stickers za visa. Hizi stickers za visa ni kichaka ambacho kinagharimu Taifa letu hasara kubwa. Wale Maafisa wa Uhamiaji ulikuwa ni mradi wao wa kujitengenezea mabilioni.

Mheshimiwa Spika, walikuwa na mambo mawili; mwaka 2019 CAG alienda pale kufanya special audit tena ilikuwa ya interval ndogo ya miezi sita, kuanzia Januari mpaka Juni, 2019, kukagua namna ya utoaji wa stickers za visa kwa wageni wanaokuja ndani ya nchi. Alikutana na maajabu makubwa sana. Alikuta kwanza kuna visa zaidi ya 33,500 zilizotolewa ni fake. Yaani wale Maafisa Uhamiaji walienda kujitengenezea hizo stickers, wakagawa, wakachukua hela, wakaweka mfukoni zaidi ya Shilingi 3,800,000,000/=, maisha yakaendelea business as usual.

Mheshimiwa Spika, walipoendelea kukagua wakakuta zaidi ya visa 21,705; zilipokelewa fedha zikaingizwa kwenye database ya Uhamiaji, baadaye wale Maafisa wakaenda kufuta zile taarifa zote kwenye database, wakachukua zaidi ya Shilingi 2,516,000,000/= wakagawana wafanyakazi 40, maisha yakendelea, business as usual. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kilichokuja kutokea sasa, Maafisa saba wakapelekwa Mahakami wakafunguliwa kesi ya Uhujumi Uchumi kwenye Mahakama Kuu Moshi. Wakakaa pale gerezani miaka miwili, baadae DPP akafanya nolle prosequi kwamba sina nia ya kuendelelea na kesi hii. Wakarudi kazini, wakaendelea kupiga maisha. Tuki-audit mwakani tutakuta wametupiga tena Shilingi bilioni sita, business as usual. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, lazima kama Taifa tutafakari. Watu 40 wamekula vituo vya afya sita peke yao, na wamerudishwa kazini, wameingia kwenye payroll na maisha yanaendelea. Sisi tunakuja kupiga kelele hapa, tutawasadiaje Watanzania masikini tuliowaacha huko Vijijini, waliotutuma ndani ya Bunge hili? Watu wachache wananufaika na fedha za Umma.

Mheshimiwa Spika, nawaomba sana watu wa Serikalini, ninyi mliopewa dhamana na Mheshimiwa Rais, katusaidieni katika mambo haya. Kuwaachia watu wanakula fedha, wamerudi wako ofisini na hiyo audit ilikuwa ni trend a miezi sita, just imagine kama unge-audit ya miaka mitano, si ungekuta karibia bajeti ya Wizara nzima watu saba wamekula, business as usual na maisha yanaendelea! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili la Uhamiaji nadhani message mmeipata vizuri kitu gani nakusudia kusema. Nendeni mkafanye upya, mrudie na ule mfumo, hao watu walienda kufuta vitu kwenye database. Ule mfumo mmeuanzishaa upya, nendeni pia mkafanye reconciliation baada ya ku-abandon ule mfumo wa zamani: Je, huu mfumo mpya una-address yale matatizo? Au mme-create mfumo mpya ambao ni loophole nyingi kutupiga zaidi na zaidi! Kwa hiyo, nawaomba watu wa Serikali mkawe makini kuangalia hasara tuliyosababishwa, lakini watu hawa waliosababisha wizi wa namna hiyo kuwarudisha ndani ya Uhamiaji ina-send message mbaya kwa wale waliopo mle, kwamba, kumbe unaweza ukapiga hela! Mimi napokea mshahara wa Shilingi 800,000/=, mwenzangu kapiga Shilingi bilioni mbili kaenda kupumzika kidogo gerezani mwaka mmoja amerudi, tumeendelea na Shilingi bilioni mbili na hakuna chochote! Naye atakuwa attempted, atachukua naye Shilingi bilioni tano, naye ataenda kukaa gerezani mwaka mmoja atarudi nolle prosequi, maisha yataendeleea. Ndugu zangu, haya ni mambo ya kusikitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo kubwa ambalo pia niwaombe watu wa Serikali, nimepitia sana ripoti ya CAG katika area ya compliance kwenye Public Procurement Act. Yaani taasisi hii, ile sheria ni kama wameiweka huko kwenye kabati wanajiendeshea mambo. Nimeona Jeshi la Polisi pale, hata issues zao za procurement, 70% ya issues zote walizozifanya ni non-compliance na sheria. Wanaenda kulipa fedha wakandarasi bila hata kazi kukamilika, Auditor anaenda kukuta fedha zimelipwa na mradi haupo.

Mheshimiwa Spika, kuna Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa walinunua magari, magari yenyewe hayo yalilipiwa zaidi ya Shilingi bilioni mbili na milioni mia saba na kidogo, lakini magari yenyewe hayapo. Kwa maana hayo magari yalilipiwa hata kabla hayajawa delivered. Yaani you pay before delivery of goods. Katika bajeti hiyo, tena wame-exceed. Bajeti iliyokuwa approved na budget approving authority ilikuwa ni Shilingi milioni 388. Kwa bahati mbaya, unakuta wamefanya expenditure ya Shilingi 2,400,000,000/= bila budget approving authority.

Mheshimiwa Spika, sasa variance unayoiona hapo kwenye Shilingi 2,300,000,000/= iliyokuwa approved, variance ni kubwa sana. Sasa tuki-entertain mambo haya na tukaona hii ndiyo culture ya kuendesha mambo yetu ndani ya Serikali, tuta-create vacuum kubwa kwenye Taifa hili. Watu wataacha ku-comply, tutakuwa na hizi documents kama urembo tu na watu watakuwa hawa-comply. Kwa sababu tunaweka wenyewe sheria, badala ya kuzifuata, tunaweka kwenye makabati, tunaanza kutumia sisi wenyewe tunavyofikiria. Haiwezi kutusaidia.

Mheshimiwa Spika, nimeona pale TTCL kwenye manunuzi, yaani ni wezi. Tuombe PPRA ikafanye special audit kwenye mashirika haya ambayo tumeona. Compliance kwenye Sheria ya Manunuzi ni mbaya. Compliance siyo ile ambayo, inaishia tu kwamba tume-comply, ni compliance ambazo zina impact kwenye finance. Kwa sababu unakuta umesaini mkataba na mtu, hakuna power of attorney, kwa maana ule mkataba is null and void. Mmempa kazi, kesho na kesho kutwa asipo-perform hamwezi kumshitaki. Hakukuwa hat ana mtu aliyepewa power ya kisheria ya kusimamia mkataba wa Shirika. Shirika kubwa kama TTCL yanafanyika mambo ya ajabu kama haya. Nawaomba ndugu zangu, kuna issues nyingi sana kwenye compliance ya manunuzi. Nendeni mka-scrutinize document ya CAG muone weight ilivyo na significant impact itakayotupelekea. Kutakuwa na issue za litigation, tusipoona hapa tutashtakiwa.

Mheshimiwa Spika, kuna mkataba mmoja nimekuta pale TTCL wa Shilingi bilioni tano. Wamesaini ule mkataba na Mkandarasi alitakiwa amalize ndani ya miezi ya mitatu, ilikuwa ni kutengeneza ule mfumo wa short sms, lakini mpaka leo una zaidi ya miaka tisa hajawahi kumaliza. Nikawauliza sasa position ya mkataba kama huu ni upi? Yaani yeye alitakiwa awakabidhi kazi ndani ya miezi mitatu, lakini amechukua zaidi ya miaka mitano na mnaendelea na maisha na mnasema this is good, let us live, business as usual.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa mawazo yangu niliyotumwa na wananchi wa Jimbo la Kwela katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu kwa kazi nzuri wanayochapa katika Wizara hii, wataalam wa Wizara hii pamoja na Kamati ya Bunge inayosimamia Wizara yao kazi ni nzuri, niwape pongezi zangu za dhati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi zangu, naomba niwakumbushe Mheshimiwa Naibu Waziri na Waziri hapo. Mnamo tarehe 12 Februari niliuliza swali kuhusu mgogoro wa Uwanda Game Reserve kule katika Jimbo langu la Kwela. Huu mgogoro umetutesa sana wananchi, hasa wa Kata ya Kapenta, Nankanga, Kilangawani na Kipeta baada ya hili pori kuchukuliwa na askari wa TAWA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanzo lilikuwa linamilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, mwaka 2013 walipochukua ndio matatizo yalipoanza, maisha ya wananchi yamekuwa ya mateso miaka saba. Naibu Waziri ni shahidi, kila wiki nampigia simu zaidi ya mara mbili nampelekea migogoro, nashukuru ananisaidia, wananchi wangu juzi walinyang’anywa mipunga na askari, wamerudishiwa. Pia wavuvi wale wa Forodha ya Nankanga waliokuwa wamelazimishwa walipe shilingi milioni nane, Waziri ameingilia kati hawakulipa zile shilingi milioni nane. Nawapongeza kwa jitihada hizo ni nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hii ni ad hoc solution, tunatakiwa tuwe na permanent solution. Baada ya askari wa TAWA kuchukua pori lile mipaka ilivurugwa, haieleweki, kwa hiyo, wananchi wamebaki dilemma kwa miaka saba. Wamekuja Mawaziri waliowatangulia wanaahidi na wakawaambia wananchi tumeunda timu ya Mawaziri saba tutawapa majawabu, mimi nimekuwa nikifuatilia hayo majawabu sijayasikia, wananchi wako hawajui kinachoendelea. Kwa bahati mbaya hii Uwanda Game Reserve hata wanyama wenyewe sio wengi, wako tembo wanne na nyati wawili tu na kwa miaka minne iliyopita tumepata watalii wawili tu, for four years watalii wawili. Kwa hiyo, imekuwa ni cost generation centre rather than revenue generation centre. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri, kutokana na mabadiliko ya tabianchi Ziwa Rukwa linakua, limekua mpaka limeingia kwenye hifadhi, wavuvi wakiingia kuvua kwenye hili wanawakamata…

T A A R I F A

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Cecil Mwambe.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa Taarifa mzungumzaji kwamba kilichopo kwenye hiyo game reserve anayoitaja, tuna game reserve pia nyingine iko Masasi DC inaitwa Misyenjesi. Wananchi wanatamani waachiwe lile eneo wafanye shughuli zao za kilimo kwa sababu haina manufaa yoyote kwao na hakuna wanyama pale ndani.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Deus Sangu, unapokea Taarifa hiyo?

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naipokea hiyo Taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nitoe ushauri kwa Wizara hii, waliniahidi kwamba, tutaenda kutembelea hili pori. Nashukuru, nasubiri hiyo ahadi yao na aliniahidi Waziri kwamba, tukimaliza bajeti hii tunaenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, wavuvi wanakamata vifaa vyao. Boti ukilichukua ukalitoa kwenye ziwa ukaweka nchi kavu miaka mitatu, baada ya hapo wakifanya mnada inakuwa ni kuni, inakuwa hasara kwa mvuvi pia inakuwa hasara kwa Serikali, hakuna kitu kiinachozalishwa pale. Kwa hiyo, niwaombe sana ili tuondoe migogoro hii na kufanya ile Uwanda Game Reserve tutoe vibali kwa wavuvi wakavue kwa vibali, kwa sababu kitendo cha kutotoa vibali mmewahalalishia askari waanze kuchukua rushwa. Mvuvi anatoa shilingi milioni moja, hela zinaenda kwa mtu binafsi, Serikali hawapati chochote, si bora watoe vibali ili waingize fedha katika Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe sana Wizara hii. Migogoro hii hata Rukwa Lukwati kule kuna mgogoro wa aina hii, wavuvi wananyanyasika sana. Wavuvi wanakuwa charged mpaka shilingi milioni tatu, hizo fedha wanachukua askari binafsi, Serikali haipati hata senti moja, mateso ni makubwa, wananchi wameumizwa sana. Niwaombe sana watakapokuwa wana-wind up watoe kauli, migogoro ile wataimaliza lini ili la wananchi wa Kata ya Nankanga, Kapenta, Kipeta, Kilangawane, wafurahie kwamba, kuwepo kwa ile Uwanda Game Reserve kuna faida kwa sababu, wanatusaidia katika bio diversity conversation. Wamekuwa wakitusaidia pamoja na kwamba hamna watalii, lakini pia utunzaji wa mazingira, lakini wananyanyasika sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kuchangia kwa njia ya maandishi kwenye bajeti hii muhimu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kutoa ushauri muhimu sana hasa juu ya mgawanyo wa fedha za miradi zinazoletwa katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais juu ya fedha nyingi zilizoletwa kwenye jimbo langu la Kwela na hivi karibuni tumepokea fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na shule kwa shule za misingi. Kwenye Jimbo langu nakiri Halmashauri yangu kupokea fedha kwa ajili ya shule mbili zenye mikondo miwili ambapo Shule ya Motowisa A tumepokea shilingi 538,500,000 na Shule ya Tuwi iliyopo Ilemba B imeletewa shilingi 538,500,000.

Mheshimiwa Spika, pia fedha kwa ajili ya madarasa na vyoo kwenye Shule ya Laela B shilingi 75,000,000, Shule ya Kisa Kata ya Milepa shilingi 75,000,000, Shule ya Nankanga shilingi 100,000,000, Shule ya Kaoze shilingi 69,100,000, Shule ya Kinambo Kata ya Milepa shilingi 75,000,000 hivyo kufanya jumla kuu kuwa shilingi 1,497,100,000. Tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kupokea fedha hizi naomba kuleta kwako Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI mapendekezo ya mgawanyo wa madarasa kwa awamu zijazo kwani Jimbo la Kwela ni kubwa sana lina kata 27 na kila kata wamejitahidi sana wamejenga maboma ya zaidi ya miaka mitano. Ushauri wangu kwamba kwa wakati mwingine Serikali ione kuna haja ya kufanya mgao walau kila mahali waweze kupata kidogo kwani shida na uhaba upo kila mahali ndani ya Jimbo la Kwela.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano maeneo ambayo mmepeleka fedha za BOOST ndio hayo hayo yalipata fedha za SEQUIP kwenye sekondari. Hii inapelekea maeneo mengine kuona kama wametengwa. Pamoja kwamba mnaweza kuwa mnatumia takwimu, lakini suala la kuleta usawa ni muhimu sana kwani kila eneo wanataka kupata walau fedha kidogo toka Serikali Kuu.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumuomba Mheshimiwa Waziri wakati mwingine wanapotaka kupeleka fedha za miradi huko majimboni watushirikishe ili tuweze kushauriana, tofauti na sasa hivi wanaleta fedha ambayo badala ya kutuleta pamoja inasababisha mipasuko ya kimaeneo hasa kwa majimbo yetu kama Jimbo la Kwela ambalo jiografia yake ni ngumu sana. Kwa mfano awamu hii ya BOOST mapendekezo yetu hayakuzingatiwa na Wizara kabisa badala yake wametumia takwimu zao walizonazo Wizarani. Kwa mfano mapendekezo yetu ya mradi ya BOOST yaligusa kila eneo kwa kuzingatia uhitaji wa maeneo kama nilivyoaanisha kwenye jedwali hapa chini.

Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Mapendekezo ya bajeti ya ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa fedha za Programu ya Elimu ya Lipa kwa Matokeo (EP4R/BOOST) kwa mwaka 2022/2023.

JEDWALI

Mheshimiwa Spika, naomba sana Wizara ingalie namna ya kugusa maeneo yote kama nilivyoainisha ili kila eneo au kila kata wapate walau madarasa mawili au matatu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na ahsante sana.

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye hoja zilizopo hapo mezani. Kwanza kabisa niungane na wenzangu kukupongeza kwa nafasi hii ya kuwa Spika wa Bunge pia nimpongeze Naibu Spika. Lakini kwa namna ya pekee nizipongeze oversite committee zote kwa maana ya PAC na LAAC kwa presentation ya Wenyeviti wake wamefanya presentation nzuri sana niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitajikita kuchangia hasa kwenye benki zetu za Serikali nataka nielezee going concern ya benki zetu za Serikali. Serikali kuwa na benki zake yenyewe ni jambo muhimu sana, lakini kuanzia mwaka, 2017 Serikali ilichukua uamuzi wa kuunganisha benki zake. Kwanza, ilianza kuichukua TWIGA kuiunganisha na Benki ya Posta; baadaye ikaja kuchukua Benki ya Wanawake ikaiunganisha mwaka, 2018 na Benki ya TPB. Shida kubwa hizi major mbili hazikuwa na tatizo kubwa shida kubwa ilikuja pale ambapo, Serikali iliamua kuchukua benki ya TIB Corporate na kuiunganisha na Benki ya TPB ili kuunda Benki ya TCB ambayo ni Benki ya Biashara ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo lilikuwa ni zuri labda tulikuwa tuna-revert will yetu ya kubinafsisha Benki ya NBC ili tuwe na Benki ya Biashara ya kwetu ya Serikali, lakini kitendo cha kuileta TIB Corporate tayari ilikuwa na mikopo chechefu ya Shilingi bilioni 130, hii imekuja kuharibu mizania ya vitabu vya, Benki hii ya TPB ambayo ilikuwa tayari ipo kwenye top ten ya benki zinazofanya vizuri hapa nchini. Kwa sababu, tuna benki sasa zaidi ya 50 lakini benki yetu ya Serikali ya TPB ilikuwa ina- perform vizuri. Kuleta kwa mikopo chechefu na pia ikaleta mzigo wa wastaafu kwa maana ya staff management team ile ambayo ilikuwa na mishahara mikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka leo kutokana na ofisi ya Treasurer kuto-solve huu mtanziko pale ndani ya benki ni kama kuna management mbili. Kuna wale waliotoka TIB Corporate ambao wage bill yao kwa mwezi inakwenda, 1.7 billion shillings ambao kazi kubwa inayokwenda pale ni kusoma magazeti. Unalipa shilingi 1.7 billion kwa mwaka fedha za walipa kodi hawajapangiwa majukumu, sasa inaonekana Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina hawakujipanga wakati wanafanya hii merger. Ilitakiwa watumie approach ile waliyofanya wakati wanabinafsisha ile Benki ya NBC, walichukua madeni na mali zile ambazo, wale makaburu hawakuzitaka, wakaunda Shirika pembeni tanzu la CSC kwa ajili ya ku-deal na yale mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa huku approach ilikuwa wakapeleka madeni mabaya Shilingi bilioni 130 na Treasurer aliji-commit kwamba huu mzigo nitaubeba. Tangu Juni, 2020 ameweza ku-recover Shilingi bilioni tatu tu, kwa hiyo itamchukua zaidi ya miaka 40 ku-recover ile mikopo chechefu. Ile mikopo mingi, ukiiona haina future yoyote, mikopo ile yote yawezekana hata Serikali isiweze ku-recover zile fedha. Sasa, naomba kuishauri Serikali kuna approach mbili ambazo unaweza kutumia kuisaidia benki hii, ambayo ina matawi 83 na ina wakala wa benki zaidi ya 3,500 nchi nzima na ni benki ambayo tunaitegemea kama Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza; wakubali kuchukua ile mikopo iondoke kwenye mizania ya vitabu vya Benki ile ya TCB. Pili, hawa management ambao wanalipwa Shilingi 1.7 billion na wapo tu wanasoma magazeti, watafutiwe sehemu nyingine ndani ya Serikali, kuna mamlaka nyingi, wakafanye kazi, kuliko kutumia fedha za walipa kodi hawafanyi kazi yoyote. Hii contradiction tu ni basi tu katika making decision, ilitakiwa siku ile tu ya merger wawe wameamua hili jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, tuna benki yetu nyingine kubwa kabisa Benki ya Maendeleo ambayo ni TIB Development katika nchi yoyote ile kwa mfano China Development Bank. Hii China Development Bank ndio ina- finance miradi yote mikubwa ya kimkakati ndani ya nchi ya China, lakini sisi hii TIB Development alipoianzisha Mwalimu Nyerere mwaka 1970 alikuwa na nia njema. Kukaingia ulaghai na ujanja ujanja mpaka ninaposema leo hii mikopo chechefu imefika Shilingi bilioni 327 na kila mwaka wakijitahidi wanakusanya labda shilingi bilioni mbili au tatu. Maana yake hata benki hii leo hii ukienda wame-stop lending hawakopeshi, kwa sababu, fedha ina liquidity crisis maana yake ni nini kinachoweza kutokea hapo?

Mheshimiwa Spika, wamesema watatoa non cash bond. Noncash bond ni kwenda tu kuweka mizania ya vitabu ikae vizuri, lakini hai-address tatizo la mtaji la benki hii. Ina mtaji wa Shilingi bilioni 38, lakini requirement ya Benki Kuu inatakiwa Benki aina ile ya TIB Development iwe na mtaji wa shilingi bilioni 50. Sasa, leo hii unakwenda kufanya non cash bond ambayo pia inakwenda na impact kwenye deni la Taifa, tayari hata TCB wanasema, wanakwenda kuweka non cash bond, yes ni initiative ya kuweka mizania ya vitabu, isome vizuri, lakini hai-address matatizo ya benki zetu hizi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali kama inataka kweli twende mbele kwenye financial sector na hapa sijaongelea Benki ya Maendeleo ya Kilimo nayo hali ni hii hii. Maana yake sisi ndio tuna-prove failure; Benki Kuu inasema asilimia tano ya non-performing loan against assets zako ndio inatakiwa, lakini sisi kwa mfano, TIB leo mikopo chechefu ni zaidi ya asilimia 50 wakati inatakiwa iwe asilimia tano, tunakwenda wapi tumeamua kuua benki zetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa sababu ya muda niishie hapa. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii ili niweze kuchangia kwenye Sekta muhimu sana ya Kilimo. Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri Bashe na Naibu wake kwa kazi nzuri wanazofanya pale Wizarani. Katika Wizara hii nitakuwa na mambo muhimu matatu: Kwanza nitaongelea kampuni yetu ya mbolea ya Taifa kwa maana ya Tanzania Fertilizer Company; muda ukiniruhusu nitaongelea Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko; na mwisho kabisa nitamkumbushia Mheshimiwa Bashe ahadi zake alizotupa wakati alipofanya ziara Mkoani Rukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Kampuni yetu ya Mbolea, Mheshimiwa Bashe anajua wazi na kwenye bajeti yake leo hii amesema kwamba wanaenda kuiongezea uwezo Kampuni yetu ya Mbolea ya Taifa kwa maana Tanzania Fertilizer Company bilioni 6.0. Hata hivyo, nimkumbushe, kampuni yetu hii bilioni 6.0 aliyotaja hapa leo, ni token tu, tuna tatizo kubwa na ndiyo instrument kubwa ya nchi hii ambayo itatusaidia katika ku-stabilize bei za mbolea nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 2008 tulipoiacha hii kampuni ikafa kwa sababu ya mbolea ya ruzuku isiyolipika, tukaitwisha mzigo wa madeni mengi, hii kampuni ya mbolea ikafa, tumewaacha private operator wana-operate soko la mbolea, tatizo lake ni nini? Wanaweza wakafanya curtail, wakafanya inflation na ndiyo maana unaona bei ya mbolea nchini imekuwa haitabiriki. Kama kampuni yetu ingeweza kuwa na fedha, kama kampuni yetu ingekuwa ina uwezo, tungeweza angalau kama Serikali tukasimama, wakati wa migogoro na shida ya mbolea kama leo, kampuni hii wangeweza wakafanya kazi hiyo pasipo tatizo lolote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ninavyoongea Waziri ametaja bajeti yake bilioni 6.0, wakati huo hii kampuni inawadai watu, Serikali bilioni 3.0, vyama vya ushirika bilioni 2.0, watu private zaidi ya bilioni 10 na na kitu. Kwa hiyo jumla ya bilioni 19 ziko kwa watu. Mheshimiwa Waziri anahangaika tumpitishie bilioni 6.0 hizi, lakini kuna bilioni 19 watu wapo, hawajafa, wapo na wanaendelea kuwepo. Mheshimiwa Waziri atumie Serikali ina mkono mrefu, watu warudishe bilioni 19 tufufue kampuni yetu ya mbolea kwa sababu bila hivyo tatizo la mbolea litatusumbua sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamesema kwamba hatuna hata stock ya mbolea, lazima tuwe na buffer stock ya mbolea kwa sababu bila hivyo ukitegemea private operator wao wanafanya kwa kufuata theory ya just in time. Akileta mbolea anauza, hawezi kuweka stock ya miaka miwili au mitatu kwa sababu yeye siyo shughuli yake, yeye anataka apate faida kwa wakati huo, akishapata faida anaachana na mambo hayo. Hivyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri aende kufanya shughuli hii ya kuwafuatilia wale waliochukua bilioni 19 kwenye kampuni yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa mara ya kwanza ameonyesha nia njema na kampuni hii. Amelipa madeni bilioni 9.0 kwenye Benki ya Exim, lakini bado tunadaiwa bilioni 15 kwenye mabenki mengine. Mheshimiwa Waziri aende kupambana kwa namna yoyote, tutakapoenda kupeleka ruzuku ya bilioni 250 alizotaja hapa, kampuni yetu iwe imefufuka nayo ishiriki ili isaidie ku-regulate suala la mbolea. Wananchi wangu kwa mfano Mkoa wa Rukwa tumehangaika, tumeshindwa hata kulima mahindi kwa sababu mbolea ilikuwa juu. DAP tulikuwa tunanunua mpaka mfuko mmoja Sh.150,000; UREA imeenda Sh.85,000, bei ni kubwa, wananchi waliamua waachane na mahindi. Hivyo, Nimwombe sana Mheshimiwa Bashe, nataka nijue atakapokuwa anahitimisha atupe strategy, aachane na hiyo bilioni 6.0, ni namna gani anafufua Kampuni yetu ya Mbolea ya Tanzania. Hilo ni jambo la kwanza nilisema nitalisemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni Bodi yetu ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko. Inatusaidia sana kutafuta masoko, tumepata masoko ya mazao kule Sudan ya Kusini, Rwanda, Zimbabwe, Comoro na DRC. Sasa suala la DRC kwa kwetu Mkoa wa Rukwa ndiyo soko letu la Jirani, lakini linakumbwa na vikwazo vingi sana kwa sababu lazima tupite Zambia na pale Zambia nao ni competitor wetu kwenye zao la mahindi wanatuwekea trade embargoes ambazo zinafanya biashara ile iwe ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri Mheshimiwa Bashe kupitia Wizara ya Mambo ya Nje, yeye mwenyewe na Ubalozi wetu wa Zambia, waende wakaongee na Serikali ya Zambia watupunguzie hivi vikwazo kwenye mazao, yaani mfanyabiashara akitoka na mazao kwa mfano Songwe, Rukwa akifika tu Zambia wanaweza wakamweka hata wiki mbili au wiki tatu. Mambo mengine kama samaki na mazao mengine hawana shida, ila zao moja tu la mahindi ndiyo kikwazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe na Waziri analijua vizuri jambo hili, kupitia ubalozi wetu, Wizara ya Mambo ya Nje, tukafanye kupitia diplomasia yetu na nchi jirani ya Zambia wasitunyanyase kwenye zao la mahindi, kwa sababu wamekuwa wakitoa visingizio kwamba mahindi yetu yana sumu, wafanyabiashara wanapata hasara wakiwa hapo hapo na mwishowe wanakata tamaa, kwa hiyo mazao yetu hayapati fursa ya kwenda huko DRC pale Lubumbashi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kwenye hii Bodi ya Mazao Mchanganyiko, nimefanya utafiti na mpaka tukafanya mazungumzo na Jimbo jirani la Out Katanga, wametushauri jambo moja hii habari ya kupita nchi za jirani ndiyo maana tunapata mateso, tukae na Wizara ya Fedha, tutafute mwekezaji, tutengeneze zile kilometa 720 ambazo zitatupeleka Lubumbashi, ambayo itatupa fursa sasa ya kufunguka kwa Bandari ya Kasanga, Bandari ya Kalema na Bandari ya Kabwe, tutaenda kwa urahisi kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukipata mwekezaji atawekewa fee ya barabara ambayo return yake haifiki hata miaka mitano, yule mwekezaji pesa itarudi na barabara ile itafungua Mkoa wa Rukwa, Katavi na Kigoma. Nimwombe sana Mheshimiwa Bashe, haya manyanyaso ninayomwambia ya kupitia nchi za jirani sasa tukafungue. Tumewekeza bandari nilisema hata kwenye hotuba ya Waziri Mkuu, bandari zile zinabaki kuwa idle. Twende tukamalize tu kilomita 720 tuunganishe pale Bandari ya Moba, upande wa pili wa Zambia, tukafike Lubumbashi ili ghala lile linalotunza zaidi ya tani 2000 kule Lubumbashi liwe na impact na Bodi ya Mazao Mchanganyiko waone tija kwamba kweli tumeenda kusaidia kutafuta masoko kwa ajili ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo nataka niongelee pia ni kwamba, hii bodi tumeipa majukumu mazito ya kuchukua viwanda vilivyokuwa chini ya NMC. Ili viwanda hivi viweze kuongeza thamani ya mazao ya wakulima wetu na nimwombe Waziri, mikoa mingine imeweka vinu vya kusindika mpunga, mahindi, lakini Mkoa wa Rukwa sijaona. Nimwombe sana Mheshimiwa Bashe na amekuja pale, tupate na sisi kiwanda walau cha kusindika mpunga, tupate viwanda vya kusindika mahindi ili tuongeze thamani ya mazao yetu ambayo yatafanya wananchi wetu wapate urahisi wa kupata masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna shida moja na naomba hii Waziri wa Fedha popote alipo anisikie. Bodi ya Mazao Mchanganyiko wameandika proposal kuomba kuendeleza hivi viwanda na ile proposal inataka tu approval kutoka Wizara ya Fedha. Approval ile imekuwa na vikwazo na ile siyo government guarantee ni just a government concept, wana-approve tu, wanatupa fedha na ile fedha haina impact yoyote kwenye deni la Taifa, yenyewe inaenda kufanya jambo moja kwamba mnakuwa na partnership na Benki, CPB na Benki wana-operate kiwanda, Benki ikipata revenue yake wanawaachia kiwanda kinakuwa cha kwenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwomba sana Mheshimiwa Bashe, watakapokuwa hata kwenye Baraza la Mawaziri amweleweshe vizuri najua ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ni Economist anajua, hili jambo halina impact yoyote kwenye deni la Taifa, ni jambo tu la ku-approve, wachukue hizo fedha, wajenge viwanda vya kuongeza thamani za mazao kwa mwananchi ili tuweze ku-compete. Mwezi Machi Mheshimiwa Waziri alikuwa yuko kwenye maonyesho ya Dubai expo, sasa masoko yatakuja mengi, baadaye hatutaweza ku-compete kwa sababu hatuna value addition ya mazao yetu. Nimwombe sana Waziri, hili jambo ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu na la mwisho sasa, nimkumbushie ahadi alizokuwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umekwisha, malizia kwa dakika chache malizia.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi zote za Mheshimiwa Bashe nitampelekea kwa maandishi na nitataka kujua status ya hizi ahadi alizoahidi zitaishaje, maana ana ahadi kama 10, naona ametekeleza mbili tu, ahadi nane bado namdai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi na mimi nitoe mchango wangu kwenye Bajeti Kuu ya Serikali. Nianze kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya katika Taifa hili lakini kipekee kwa miradi mikubwa anayoifanya ndani ya Jimbo langu la Kwela na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla sisi tunampongeza na tunamuombea maisha marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Naibu na timu yote ya wataalamu niwape pongezi kubwa kwa kazi kubwa mnayofanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais. Leo pamoja na mambo mazuri yaliyosemwa katika Speech yako ya Bajeti Mheshimiwa Waziri nina mambo machache ya kushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja ambalo nililifurahia ni kati ya Wabunge waliosimama kuchangia juu ya hali ya mtaji kwenye Benki zetu za Serikali kwa maana ya TCB (Tanzania Agricultural Development Bank) pamoja na TID Development. Nimeona katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri mmetenga kiasi cha shilingi bilioni 235 kwenda kuziwezesha benki hizi ili walau kuzinusuru katika hali ya mtaji lakini kwa namna ambayo nimeona plan yenu ya kutenga shilingi trilioni moja ndani ya miaka 10 ili kila benki hizi tatu ambazo ni benki za kimkakati za Serikali ziwe na fedha au mtaji wa shilingi trilioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo jema lakini muda mliojiwekea miaka 10 ni muda mrefu sana. Ninachoomba mfanye kwa TCB mmetanguliza fedha shilingi bilioni 30 na hivi karibuni mnaenda kupeleka shilingi bilioni 101. Jambo hili nawapongeza kwa fedha hizi mnaenda kuinusuru hii Benki inakaa vizuri kimtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo deficit ambayo tunatakiwa kuweka pale ni shilingi bilioni 700. Katika Bajeti hii mnapeleka shilingi bilioni 100. Niwaombe ndani ya muda mfupi mfikishe hii shilingi trilioni moja kwenye Benki hii ya Kilimo ili kusiwe gap kubwa kwa maana huu mtaji mnaoweka shilingi bilioni 100 msipokaa vizuri mkasubiri hiyo miaka 10, nao utamezwa kutakuwa ni kazi bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika Benki ya TID Development (Benki ya TID Maendeleo). Ile pale ina deficit ya mtaji karibia shilingi bilioni 370. Napo pale mnapeleka shilingi bilioni 100, kutabaki deficit karibia ya shilingi bilioni 270. Naomba nazo hizi mzitengee muda mfupi mkakamilishe, mkishindwa kufanya hivyo maana yake hata shilingi bilioni 100 hii itamezwa kutakuwa ni kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkifanya hivyo wazo la kuja na shilingi trilioni moja litafuata baadaye wakati tayari mme-stabilize vitabu katika Benki hizi hizi tatu za Serikali. Ni jambo muhimu sana nililotaka kushauri Mheshimiwa Waziri na ulichukulie kwa maanani makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo limepigiwa kelele ni suala la ununuzi wa mazao nitaongelea zao la mahindi na Mheshimiwa Waziri Bashe kwenye bajeti hii umesimama zaidi ya mara nne, mara tano umetoa maelezo mazuri kabisa sina mashaka naye. Umetoa maelezo na ulivyosema kauli yako unasema kwamba hatufungi mipaka lakini mnataka m-regulate export ya mahindi mkuze wigo wa kodi (tax base) ili tayari export ya mahindi iwe reflected kwenye mapato ya Taifa ni jambo zuri lakini mnapofanya hiyo approach muangalie pia stabilization ya price kwenye zao hili la mahindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya wiki mbili hizi ambapo mko kwenye transition period hapa mahindi yalikuwa kilo moja shilingi 800, hivi ninavyoongea ndani ya wiki mbili hapo ambapo mnakuja na hizo measures za ku-control export ime-drop kwenye Mkoa wa Rukwa kutoka shilingi 800 mpaka shilingi 450. Maana yake gunia la shilingi 80,000 lime-drop mpaka shilingi 45,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni nini? Chochote unachowaza kufanya, control measure yoyote unayofanya iwe ya kudhibiti export ya mahindi ili nayo ichangie kwenye kodi ya Serikali siyo jambo baya, hakikisha stabilization ya price ya mahindi isiyumbe kwenye measures unazochukua. Kufanya hivyo hakutakuwa unachofanya, madhara yake yako kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaenda huko mtaweka hizo sijui control, sijui hivi masharti mengi mengi, mta-discourage hawa wanaotaka kununua mahindi yetu. Mkisha-discourage, competitor wetu wa zao la mahindi mkubwa ambaye anafanya vizuri katika viwango vya juu ni nchi jirani ya Zambia. Ita-capitalize masoko hayo na baadaye hata tuje tufungue mipaka, tupunguze nini hatutaweza kupata wateja wa mahindi yetu yatakuwa tayari zao la mahindi lime-collapse. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii siyo kwamba ni mara ya kwanza itatokea, hapana. Mwaka 2017, 2018, 2019 tulifanya jambo hili hili tukafunga mipaka kwa nia tu moja tu ya usalama wa chakula nchini kwa gharama ya mkulima yaani tunataka tuwe na food security kwa expense ya mkulima. Tukafunga mipaka, tulipofunga mipaka Zambia ika-take over masoko yote ya mahindi. Soko la mahindi likaanguka, tulikuja Bungeni hapa tukapiga kelele Wabunge wote wa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini tukajenga hoja hapa ikalazimika twende tukachukue overdraft ya shilingi bilioni 50 CRDB tukanunua na bado Serikali haikuwa na capacity ya kununua kwa sababu mazao yalikuwa yamezagaa hakuna kwa kupeleka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, measures zote mnazochukua we must be very sensitive. Tuwe tuna balance, tuna balance hicho tunachosema food security ya nchi lakini tunaangalia mkulima tusimuumize kwa sababu unakuta tunafanya haya yote 45, wakulima wameshindwa kukopesheka mahindi mwaka huu. Hamna benki iliyojitolea, commercial bank zote hata Benki ya Kilimo ilikataa. Unakopeshaje zao la aina hii ambalo lenyewe halitabiriki? Benki gani inataka kupata hasara? Hamna benki inayomweza kukubali mambo ya namna hii kwa sababu hata ukiangalia Ripoti ya BOT, performance kwenye Sekta ya Kilimo mikopo imekuwa ikiyumba sana kwa sababu ya sera zisizotabirika kwenye mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alizeti Wabunge wengi wamesema wa Singida na wengine ilikuwa ni zao ambalo tulili-encourage wakulima walime na ukienda kwenye portfolio ya Benki ya Kilimo walitoa viwanda shilingi milioni 700, 800. Leo hii mikopo ile hailipiki tayari tunaenda kupeleka non-performing loan nyingi kwenye Benki ya Kilimo kwa sababu ya sera hizi zisizotabirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kodi zetu tuanvyo-set hizi kodi hizi Mheshimiwa Waziri umesema aah tunapunguza mafuta ghafi ya kuingia nchini mjue huko huko benki zetu mnazopeleka huu mtaji mlikopesha wakulima. Tutarudi mwakani benki mitaji ime-collapse kwa sababu hakuna repayment kwenye Sekta ya Kilimo tumei-paralyze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili jambo mliangalie kwa umakini mkubwa muende mkaangalie tu-balance mazao hasa mahindi tusikubali wananchi kwa mara ya kwanza wanavuna wakiwa na shilingi 80,000 leo hii shilingi 45,000. Niombe tu utakachofanya chochote Mheshimiwa Bashe iwe between shilingi 75,000 na wewe mwenyewe unasema NFRA nimeona kwenye Hotuba ya Waziri mnaenda kununua tani laki nne lakini kwenye mfumo tu wa NFRA una ambiguity na una anomalies nyingi sana ambazo zinakwanza kwenye manunuzi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza moja, hamna infrastructure za kutosha, vituo tu vya kutosha vya kukusanya mazao ya wakulima havitoshi kwa sababu inabidi mkulima asafiri kilometa nyingi kuja kufuata NFRA ilipo. Jimbo langu la Kwela unajua kwa mfano mtu anatakiwa asafiri kilometa 100 na zaidi kufuata kuuza unakuta anaenda kuuza tena anaondoka pale anakuta tena pale kuna bureaucracy nyingi. Watu wenye nguvu za fedha wanateka masoko, wao ndiyo wanakuwa wa kwanza kupima. Mkulima anayepeleka mahindi kwenye toroli kamwe hawezi ku-access NFRA kwa hiyo, niombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia bado wananchi wamekuwa wana complain hata vipimo vinavyotumika pale sehemu nyingi tuna analogia. Wakulima wanakuwa wananung’unika tuna punjwa. Nendeni hata NFRA na CPB taasisi zako mtakazoenda muende na mizani ya digital ili mkulima asiibiwe mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu kwa sababu tumeona zao la mahindi ni tija, kwa nini tusiendelee ku-pump hela nyingi? Siyo lazima tuchukue huko, twendeni kaongezeni overdraft na nyie mnunue kwenye competitive price mahindi kuliko haya mambo mengi tunayoongea ni mazuri tu ni lugha very cosmetic lakini implication yake kule siyo hivyo Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimekwambia very frankly na hiyo measure tukachukue tuhakikishe mkulima wa mahindi hatumuumizi tukanunue bei ya kuanzia shilingi 75,000 na kupanda. Chini ya hapo ni maumivu. Tuli-subsidize mbolea maana yake nini?

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sangu, taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Swalle.

TAARIFA

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Deus Sangu kwamba hii bei ya mazao ya wakulima wameuza bei nzuri ya shilingi 800, 700 kwa kilo shambani na yako mashamba yako umbali wa kilometa zaidi ya 150 kwenye masoko ya NFRA kwa hiyo, tukisema wakapeleke huko sokoni watapata hasara. Hili Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alizingatie sana, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Deus taarifa unaipokea?

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea ni msisitizo wa jambo hili. Hili tunalo Mheshimiwa Bashe tunaendelea nalo mpaka tufikie consensus mahali ambapo kutakuwa win win, Serikali i-win na mkulima a-win. Nihame hapo nadhani message itakuwa imefika vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nililokuwa nataka kuchangia Mheshimiwa Waziri wa Fedha, ifikapo nyakati kama hizi tunapoelekea mwisho wa mwaka wa fedha mifumo yote halmashauri ina paralyze haifanyi kazi. Mfano kwenye halmashauri yangu siku 20 sasa hamna business yoyote inayo-transact. Wanasema mifumo imekwisha. Tumefika mahali tulikuwa tunachukua hata kwa wazabuni mafuta, sasa hivi hata ambulance zinaenda kukosa mafuta ya kujaza pale kuhudumia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naombeni kama inafikia hatua mnapofuga mwaka wa fedha kuna shida kwenye mifumo yenu, muwe na alternative ya ku-attend emergencies za Serikali kwa sababu hatuwezi tukasema mifumo imekufa, kwa hiyo, watu wafe mahospitalini? Kwa hiyo mambo yale basic ya muhimu yasiende? Lazima mtafute alternative ya kuwa na namna ya ku-rescue yale mambo ya dharura ili sasa isiwe kwamba mifumo ime-paralyze nchi nzima hamna kinachoenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ni mbaya kwenye halmashauri tayari kuna wazabuni, wazabuni ambao walifanya kazi. Maturity obligation zao kwa maana ya wanahitaji kulipwa sasa mifumo imefungwa tutakuja tuletewe riba ya kucheleweshewa malipo tunaingiza hasara Serikali, kwa hiyo niwaombe jambo hili utakapokuwa una wind up utueleze vizuri limekaaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze na mimi kuchangia hotuba hii ya bajeti muhimu sana hii, bajeti ya Wizara ya Ujenzi.

Kwanza nikupongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wako kwa kazi mnazofanya, lakini kipekee niombe kushukuru kwa jambo moja kubwa ambalo limefanyika kuanza ujenzi wa barabara ya Laela – Mnokola kwa kiwango cha lami ambapo tayari pesa shilingi bilioni tatu zimefika na shughuli imeanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka niongelee kwa umuhimu wa pekee juu ya barabara hii; barabara hii target ni kujenga kilometa 66 ambazo zinaunganisha Jimbo la Kwela na nchi jirani ya Zambia kwa maana ya pale Mozi katika Province ya Mbala. Barabara hii ina umuhimu mkubwa, hiki kipande tulichoanza ni kidogo sana, maana yake hapo tunapofika pale Mnokola ni kilometa chache, sasa ili tuweze kuwa na impact na tukaona hii barabara itasaidia uchumi wa Jimbo la Kwela na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla, kuna haja sasa Serikali mje na mkakati wa kuendeleza hii barabara ili ikafike pale mpakani Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani, sababu yangu ni kubwa na ni ya muhimu kwamba tuna border yetu ya Tunduma ameiongelea dada yangu hapa Mheshimiwa Fiyao, ni border ambayo inapokea mizigo mingi na imefikia mahali imekuwa imezidiwa. Sasa kitendo cha kutengeneza barabara hii tutaweza kuongeza ile speed ya mizigo ile iliyo Tunduma tukaipitisha Laela, kupitia Jimbo la Kalambo na baadaye kupitia Zambia ikafika kwa urahisi. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, barabara hii ni ya kimkakati kabisa na barabara hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, namshukuru ameanza kuitekeleza kwa vitendo na hivi ninavyoongea wakandarasi wako site. Cha msingi focus yetu juu ya barabara hii tuhakikishe inafika kwenye nchi jirani ya Zambia, tutakuwa hapo tumefanya ufanisi mkubwa ambao utakuwa na tija kwenye uchumi wa Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, nataka niongelee Barabara ya Muze – Ntendo. Tayari ilitangazwa tender tangu mwezi wa saba, ninavyoongea hivi ni mwaka mzima na katika swali langu la nyongeza juzi, nilikuuliza Waziri kwamba kwa nini huyu mkandarasi mwaka mzima hajaripoti site? Na tayari mkataba kuanzia mwezi wa tisa mwaka jana alikuwa ameshasaini mkataba wa kuanza hiyo barabara? Maana yake mwaka mzima mtu ana mkataba mezani, lakini kazi hajaanza kufanya, madhara yake ni yapi Mheshimiwa Waziri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, itasababisha huyu mkandarasi siku anafika site mkataba umesha-expire na baadae tunaanza kupigwa interest ambazo hazikukusudiwa kwenye mradi huu. Nikuombe sana barabara hii ni muhimu sana na ndio inachagiza mapato kwenye Halmashauri yetu ya Sumbawanga DC. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri mkandarasi aende kuripoti site, lakini kwenye barabara hiyo hicho ni kipande tu cha kufika Muze kilometa 37. Hii ni jumuisho la barabara ya jumla ya kilometa 200 mpaka Kilyamatundu, barabara hii ndio barabara inayobeba uchumi wa Bonde lote la Ziwa Rukwa na Jimbo lote la Kwela. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii barabara kuna kipande kimekuwa na huyu consultant aliyepewa kufanya upembuzi yakinifu mwaka wa tatu sasa no plan. Hiyo report haijakamilika na barabara hiyo ya Kilyamatundu – Muze – Ntendo mpaka Majimoto inaunganisha mikoa mitatu kwa pamoja, Mkoa wa Rukwa, Mkoa wa Songwe na Katavi n akule tayari kuna shughuli nyingi za uchumi zinaendelea pale. Tuna hawa watu wa gesi ya helium wako kule site, lakini barabara ni mbovu na ubovu wa barabara hii Engineer Kasekenya tulienda na wewe mwaka jana, ina madaraja ambayo kila mwaka lazima yabebwe na mvua na yale madaraja yanagharimu takribani shilingi bilioni tisa mpaka shilingi bilioni 10 kila mwaka na huwa hakuna option, lazima yatengenezwe kwa sababu, yakishaondoka hakuna mawasiliano popote. Kwa hiyo, solution ni barabara hiyo ya lami iweze kujengwa kwa wakati, kama alivyosema ndugu yangu Mheshimiwa Mwenisongole, barabara yake yenyewe inaishia Kamsamba ambako ni Kilyamatundu, unatoka hapo unaunganisha na Jimbo la ndugu yangu Mheshimiwa Geofrey Pinda, kule Kavuu. Tayari mtakuwa mmefanya connection ya mikoa mitatu at per kwa maana ya Songwe, Katavi na Rukwa na impact ya uchumi kwa sababu bonde lile unajua jinsi lilivyokuwa na ardhi yenye rutuba, kilimo kizuri cha mpunga, lakini Ziwa Rukwa linazalisha samaki wengi, mtakuwa mmeinua uchumi wetu kwa namna ya pekee kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine la tatu ambalo nataka niongelee na limeongelewa na Wabunge karibu wote waliosimama wa Mkoa wa Kigoma, Rukwa na wa Songwe wanaongelea habari ya uwepo wa hizo meli katika Lake Tanganyika. Ameongea ndugu yangu Mheshimiwa Assa kwa data ambazo zimetoa picha halisi juu ya umuhimu wa kuwa na meli ndani ya Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, meli ya Liemba iliondoka kwenda kwenye matengenezo, lakini Mwongozo, mpaka leo hii hatujui zitarudi lini, basi tuombe meli mpya, sisi tunafanya shughuli za kilimo, soko kubwa kama alivyosema ni DRC. Hata mapato ya bandari tunayojinasibu kwamba bandari kwa mwaka huu itaweza kuandika faida ya kuingiza trilioni moja kwa mara ya kwanza ni kwa sababu ya DRC peke yake kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, DRC ina sehemu kuu kubwa ambazo ukienda eastern part kuna sehemu ambayo unapitia bandari ya Kigoma, lakini kwenye upande mwingine wa Katanga lazima upite kupitia Mkoa wa Rukwa kwa maana ya Kasanga, upite Kabwe na Kalema kwa upande wa Katavi. Kwa hiyo, hii sio option, tumejenga zile bandari, lakini tuhakikishe kwamba sasa meli inakuja ili bandari zile tulizoweka mabilioni ya fedha ziweze kuwa na tija ya kuinua uchumi wa mikoa hii mitatu kwa wakati mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, niongelee jambo ambalo lilifanyika wakati wa zamani sana miaka zaidi ya 20 iliyopita. Kulikuwa na mpango wa kuunganisha reli ya TAZARA na Mkoa wa Rukwa kwa maana ya mpaka kufika kwenye bandari ya Kasanga na bandari ya Kabwe kwa maana ya kujenga reli inayounganisha reli ya TAZARA. Itapita katika Jimbo langu la Kwela, Laela, itapita Kaengesa itaenda Matai kule Kalambo kwa ndugu yangu Mheshimiwa Kandege na baadaye tutaunganisha bandari ya Kasanga, hii reli ni muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ile document iliyofanyiwa kazi na NDC mkaifufue upya muanze kufikiria kwa sababu tusipofanya hivyo tutawafukuza watumiaji wa bandari yetu ya Kasanga ambao ni wa DRC wataenda kwenye bandari nyingine za Namibia, wataenda bandari za Msumbiji na South Africa kwa sababu speed yetu inacheleweshwa kwa sababu miundombinu yetu bado sio rafiki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe pia ndugu yangu Mheshimiwa Engineer Kasekenya utakuwa na kumbukumbu ulipofanya ziara ndani ya Jimbo langu la Kwela, kuna ahadi za kujenga barabara kiwango cha lami kwenda Seminari ya Kaengesa, kilometa tatu mmezichukua ninyi TANROADS. Nikuombe sana hii ahadi mkaitimize kwa sababu ile ahadi ni ya Mheshimiwa Rais mwenyewe Mama Samia Suluhu Hassan, lakini pia wewe mwenyewe ulivyokuja jimboni kwangu ulijionea umuhimu wa barabara hii. Nikuombe sasa katika bajeti hii tunayoenda kutekeleza muone namna ambayo mnaweza mkakamilisha barabara hii ya Kaengesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, sio mwisho kwa umuhimu, naomba niwaombe Mheshimiwa Waziri na Naibu tunahangaika sana na Mheshimiwa Rais anahangaika sana kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Pengine unaweza kupata financing kutoka kwenye Britain Institutions kama World Bank na taasisi nyingine African Development Bank, naomba kwenye usimamizi wa fedha hii inapofika mkandarasi amefanya ile kazi tumlipe malipo yake kwa wakati. Kuweka hizi pesa na ninajua sio jambo la kawaida, haiwezekani karibia kila miradi mingi lazima kuwe na ucheleweshaji ambao tunasababisha kulipa interest kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kawaangalieni wanaofanya approval kwenye level ya Wizara au Wizara ya Fedha, yawezekana kuna ujanja fulani unafanyika ili malipo yacheleweshwe kwa makusudi baadae itokee interest, jambo hili halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais anapambana kwa namna ya pekee kutafuta fedha. Nimekupa mfano, leo hii nilikuwa naangalia kuna fedha hapa interest tulipigwa kwa ajili ya kuchelewesha malipo nina figure nyingi hapa sitaki kuzitaja sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu ya muda nitakuletea uone impact ya tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutakuwa tunapata mkopo wa kujenga, lakini tunacheleweshwa makusudi, aidha iwe katika Wizara yenu hiyo ya Ujenzi au Wizara ya Fedha. Kaeni mjitathmini kati ya Wizara hizo mbili ni namna gani mnaigharimu Serikali kwa kulipa interest kwa wakandarasi ambazo hazina sababu yoyote ile kwa sababu tuna room, mkataba unatupa, section ina-provide siku 56 anapo-submit invoice mkandarasi tuwe tunafanya tathmini. Sasa mpaka zinapita siku 56, zinafika siku 100 mpaka 160 interest ina-accrue, badae tunalipa fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nimuombe Waziri, nilikuwa nataka nije kushika shilingi kwa sababu ya jambo hili, niombe tu kalifanyie analysis ya kutosha uone ni hasara ngapi Serikali imepata, kama kulikuwa watu wamefanya uzembe, kachukue hatua ya haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hii system ya defund system ina approval nyingi. Lengo la approval ni kufanya control kwa maana mmeweka level 16, lakini kama hiyo control inaenda kutusababishia hasara ya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nendeni mkatafute level chache tu ambazo watakuwepo watu makini, wanafanya scrutiny ya documents zetu wana-approve malipo yanafanyika, ili tuepukane na interest hizi tunazolipa pasipokuwa na sababu yoyote ile, nikuombe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho sasa, sio mwisho kwa umuhimu, watu wameongea sana Mkoa wa Rukwa sisi pekee ndio hatuna uwanja wa ndege. Tuna vivutio vikubwa vya utalii kama Kalambo Falls na Uwanda wa Ziwa Rukwa kule tuna Nyanda za Lyamba Lyamfipa nzuri kabisa, lakini uwanja wa ndege ambao unaweza uka-promote utalii katika eneo hili hatuna, mwaka wa tatu uwanja wa Sumbawanga unaongelewa katika bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Waziri, tumechoka na tumekubaliana, niko na wenzangu, kwenye hili sasa tutashika shilingi tujue uwanja wa ndege wa Sumbawanga mnajenga lini ili na Mkoa wetu wa Rukwa uweze kuinuka sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahangaika mpaka tuende Songwe uwanja ambao walikuwa wanagombaniana jina. Sisi hata wa kugombania jina haupo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninakushukuru sana na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii ambayo umenipatia ili niweze kuchangia mawazo yangu kwenye hoja hii ya Bajeti ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hii tuzo aliyoipata kama Azimio la Bunge la leo lililofanyika hapa nami niunge mkono kumpongeza Rais wetu kuwa mwanamiundombinu bora. Tuendelee kumwombea, achape kazi kadri Mwenyezi Mungu atakavyomjalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya na nilifarijika sana leo alipoanza kusoma hotuba yake ndani ya Bunge amesoma kwa kumtanguliza Mwenyezi Mungu. Naamini Roho Mtakatifu atamshukia na haya nitakayoyasema leo humu ndani, Roho Mtakatifu aliyemwomba amwongoze katika kusoma hotuba yake akamwongoze pia katika kuyatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa lililofanya nisimame katika Wizara hii leo ni jambo ambalo limekuwa sintofahamu kwa takribani miaka 13 sasa. Jambo lenyewe linahusu uwekezaji wa mwekezaji aliyekuja kuwekeza katika Shamba la Malonje ambaye anaitwa Efatha Ministry. Hili jambo ukiliongelea na akifika kule Mheshimiwa Waziri, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Lukuvi pamoja na yeye akiwa Naibu Waziri, wamepigana nalo jambo hili na miaka mitano hii ilivyopita palikuwa na utulivu kidogo, lakini ninavyoongea sasa hivi jambo hili limefufuka upya na hali ni mbaya sana kutokana na huyu mwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji huyu alikuja mwaka 2009, alipewa shamba lililokuwa la NAFCO, hekta 25,000, aliuziwa kwa Shilingi Milioni 600, kwa maana hekari moja aliuziwa Shilingi 24,000. Alipofika pale yeye alikuja kama mwekezaji anayekuja kufuga na baadaye makubaliano yalibadilika kwamba yeye atafanya shughuli ya kilimo. Sasa shida ilikuja pale ambapo alianza kuingilia mipaka ya wananchi wanaozunguka shamba lake hilo hekta 25,000. Sitaki kwenda mbali kwenye historia, lakini nataka niende kwenye matatizo yaliyojitokeza kwenye uwekezaji huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na shida ya unyanyasaji kwa wananchi, analazimisha kwenda kuingia kwenye vijiji ambavyo mipaka yake haipo. Kijiji kimesajiliwa, kimepewa hati kabisa, huyu mwekezaji anaenda analazimisha hata eneo la kijiji aendelee kulimiliki yeye. Naomba hapa Mheshimiwa Waziri anielewe, siyo kwamba yule ni mwekezaji, namwita dalali na nina sababu ya kumwita dalali kwa sababu hekta 25,000 alizokabidhiwa, hajafanya uwekezaji unaofikia hata hekta 1,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile ardhi kwetu ina thamani kubwa sana. Ile ardhi inaweza kusaidia nchi kuondokana na upungufu wa zao la ngano kwa sababu ndiyo ardhi yenye rutuba kubwa. Sasa hivi nchi yetu tunaagiza ngano nje, tunatumia zaidi ya Bilioni 520 na uzalishaji wetu kama nchi tunazalisha tu tani 70,000 na mahitaji ni tani milioni moja. Eneo lile analomiliki yule Efatha Ministry linaweza likazalisha tani 44,000 na kuondoa nakisi. Ina maana nusu ya ngano tunayozalisha ndani ya nchi hii lile shamba linaweza kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yeye alikuja kuchukua lile shamba, akafanya likawa collateral, akaenda kutafuta financing kwenye financial institution, baadaye aka-deviate zile fund, hamna kinachoendelea, ni mateso kwa wananchi. Kuna wananchi wangu wa pale Sikaungwi, juzi tu ameenda na bulldozer, zaidi ya ekari 70, ameenda kukatakata mazao, tena kwa kutumia vyombo vyetu vya dola, vina-facilitate mtu kufanya uhalifu wa kukandamiza haki ya wananchi wanyonge maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja hapa leo, Wizara iliwapa wale hati na nyaraka zote toka Wizarani ninazo hapa nitakabidhi mezani. Nawaomba jambo moja, kama huyu ambaye anahodhi ardhi ambayo haina manufaa miaka 13 iko idle, wanamwona ana maana kubwa na ana muscles kuzidi Serikali, niwaombe jambo moja, wawachukue wananchi wale 5,722 wa pale Sikaungu wawatafutie eneo kama walivyowatafutia watu wa Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu hawawezi kwenda kuishi pale, hawana shamba la kulima na ni maisha yao, wale siyo wafanyakazi walioajiriwa, ajira yao ni kilimo, sasa wamempa mtu amehodhi, amechukua hati ameenda kuchukulia fedha kwenye mabenki, wananchi wanakaa hawana mahali pa ku-develop mambo yao ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe mama yangu Mheshimiwa Waziri, jambo hili lina sintofahamu kubwa. Siyo Kijiji cha Sikaungu tu, kuna Kijiji cha Sandulula, Msanda Muungano, kuna Kijiji cha Songambele Azimio, Malonje kwa ndugu yangu Aeshi na pia Mawenzusi naye atasimama atasema. Hali ni mbaya, wananchi hawaelewi jambo lolote. Mwekezaji huyu kwa nini anafugwa? Amechukua hekari 25,000, haendelezi chochote, hamna kazi inayoendelea, yuko tu pale. Sisi tuna shida, mimi nimepiga hesabu zangu, kama tungepata mwekezaji proper kwenye ardhi ile tungeweza kupata mapato kama halmashauri kwa mwaka shilingi milioni 500. Kwa miaka 13 tungekuwa tumejenga vituo vya afya 13 kutokana na mapato ambayo halmashauri ingepata kwenye shamba lile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri na Naibu nimeteta naye sana na jambo hili najua Waziri alikuwa Naibu Waziri analijua. Ilifikia hatua mpaka huyu mwekezaji anakata wananchi masikio, yaani masikio. Kuna mwananchi mmoja anaitwa Martin yuko pale Sandulula mpaka leo ni mlemavu anavyopigwa na yule mwekezaji. Mbaya zaidi kuna wananchi basi kwa sababu wana fedha na anaweza akahonga hapa na pale, aliweza mpaka kusababisha wananchi wakafungwa gerezani miaka mitano, wameenda na mahakama ikakuta hawakuwa na hatia, lakini wale wananchi wamepoteza miaka mitano gerezani. Wananchi wa Sikaungu hawana hatia yoyote, masikini ya Mungu wamerudi ni maskini, lakini kwa sababu wanajua haki yao hawaachi kupambana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suluhu labda kama Wizara itashindwa kuwatafutia sehemu ya Kwenda, wajiandae wale wananchi wako radhi 5,000 wote waje wawaue palepale, wawazike Sikaungu. Kwa sababu haiwezekani, mwekezaji huyu ana ubabe gani? Kumekuwa na vitu fulani vya ajabu mimi naviona pale, mwanzoni mnakuwa timu ya watu wengi mna-fight, baadaye unaona wenzako wanarudi nyuma kwenye mamlaka hizi hizi za Serikali. Ukishaona hivyo ujue wenzako wamepigwa mlungula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi peke yangu, mimi Deus Clement Sangu niliyechaguliwa na wananchi wa Jimbo la Kwela nitasimama peke yangu, hata ikinigharimu Maisha, kwa sababu haiwezekani wananchi wananyanyasika sana. Ule mgogoro umeleta adha kubwa, wananchi mwaka huu hawajalima na kidogo walichokuja kulima amekuja kupita na bulldozer, eti anaweka mipaka. Mipaka si pande mbili mnakaa kama kuna mipaka mnaweka? Hivi wewe unaweza ukatoka peke yako ukaja kujiwekea mipaka? Haiwezekani jambo hili! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli mbaya iliyoniudhi, naomba niiseme na kwa kweli Mheshimiwa Waziri na Waziri wa Mambo ya Ndani nawaomba sana, kauli ya mwekezaji kuja kuongea, kudharau mamlaka ya nchi hii ambayo imekaa kihalali, sitakubaliana. Akirudia tena ama zangu ama zake kule jimboni. Yeye anasema kwamba, haya, mliyemtegemea amekufa, sasa narudi na kweli miaka mitano yote; Mheshimiwa Lukuvi ni shahidi, palikuwa kimya. Siku tatu baada ya Hayati Magufuli kufa akaja halafu anatamka kauli za kudharau mamlaka halali ya nchi hii, sitakubali. Kama wa kwanza kupigwa risasi kwenye shamba lile la Wanasikaungu nitakuwa mimi Mbunge wao niliyekuja kuwawakilisha ndani ya Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wamwambie kauli za kukashfu mamlaka za nchi hii iwe mwisho. Aishie huko huko, asije kudharau mamlaka, wananchi wanampenda Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia, wanamuunga mkono, asije akafanya kwamba yeye ni mbabe kuliko Serikali. Tutamalizana huko huko site.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea kwa uchungu mkubwa, naona nchi ambavyo hatupigi maendeleo, tunalia humu Bungeni hata ndugu yangu Mheshimiwa Bashe nilimwambia haiwezekani, sisi tuna ardhi yenye rutuba, ardhi nzuri iko idle mtu mmoja amehodhi tu haendelezi, njooni tufanye maamuzi, nikamshauri Bashe amwandikie barua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna vijana wengi graduates hawana ajira, wanahangaika Jimboni kwangu. Tungeenda pale tukafanyia block farming, wakapewa mle mkopo na Benki yetu ya Kilimo. Nimeenda Benki ya Kilimo nikafanya mazungumzo, wakasema tunahitaji ku-finance kwenye sekta ya ngano, lakini watapata wapi ardhi? Kuna mabepari wamehodhi ardhi na hawaendelezi, vijana wetu wanarandaranda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, kwa kweli nitalisimamia hili…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Deus Sangu.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha tu, mama sitaunga mkono, nitashika shilingi mpaka aje atupe majawabu yanayostahili juu ya mgogoro wa lile shamba. Wananchi wa Sikaungu, Sandulula na Msanda Muungano wamenituma nije nipaze sauti humu ndani ya Bunge. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kwa kukushukuru kwa nafasi ya kuchangia kwa njia wa maandishi.
Pili, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya katika kukuza sekta ya utalii, tumeona kazi yake nzuri ya filamu ya Royal Tour.
Mheshimiwa Spika, naomba sasa nichangie hoja nilizotumwa na wananchi wa Jimbo la Kwela kwenye Wizara hii muhimu. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais, wewe na Naibu wako. Ni imani yangu na wananchi wa Jimbo la Kwela kuwa mtamsaidia vema Rais wetu.

Mheshimiwa Spika, naomba kupitia Bunge lako tukufu, niwasilishe kwako mgogoro wa muda mrefu sana kati ya wavuvi wa forodha ya Ilanga, Nankanga na Legeza dhidi ya mapori ya akiba ya Lwafi na Uwanda. Lakini pia Hifadhi ya Uwanda na Vijiji 16 vilivyopo kata ya Nankanga, Kapenta, Kipeta na Kilangawana.

Mheshimiwa Spika, utangulizi; Hifadhi ya Uwanda Game Reserve iliyoanzisha mwaka 1959 na wakoloni. Mwaka 1974 ilitangazwa kwenye Gazeti la Serikali na ikawa chini ya Halmashauri hadi mwaka 2013 walikabidhiwa TAWA. Mwaka 2014 TAWA walianza kazi rasmi kwenye Pori la Akiba la Uwanda Game Reserve. Pori la Uwanda Game Reserve linazungukwa na vijiji 16 na wakazi zaidi ya 50,000 wa vijiji hivyo ni wakulima, wafugaji na wavuvi.

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Uwanda Game Reserve wakati inaanzishwa eneo hilo lilikuwa ardhi kavu na baadae kutokana na mabadiliko ya tabia ya nchi, maji ya Ziwa Rukwa yaliingia na kuungana na nchi kavu na kuwa ziwa kwa asilimia 80 ambapo eneo hilo ni ziwa kwa sasa. Hivyo eneo la nchi kavu la pori limebaki asilimia 20 tu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mabadiliko hayo, Hifadhi ya Uwanda Game Reserve imebaki inatumia mipaka ile iliyowekwa na wakoloni haijabadilishwa hadi sasa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hali halisi kwa sasa; baada ya TAWA kukabidhiwa Hifadhi ya Uwanda Game Reserve wakulima, wafugaji na wavuvi wanaishi kwa manyanyaso makubwa kwa maslahi ya askari mmoja mmoja wa TAWA.

Mheshimiwa Spika, wavuvi wanaishi kwa shida na kupoteza mali zao na maisha yao. Kuanzia mwaka 2016 hadi 2021 wavuvi waliokufa wamefikia 40 na chanzo cha wavuvi hao kufa ni askari wa TAWA. Wapo waliojitosa majini kwa kuogopa kipigo kutoka kwa askari. Mvuvi anaona bora ajitose majini kuliko kukamatwa na askari. Pia wapo wavuvi waliokamatwa na waliopigwa sana na wengine kupata ulemavu wa kudumu. Wapo wavuvi waliopigwa risasi na kufa kwa sababu ya kunyang'anywa samaki wao walipojaribu kuzuia samaki wao wasinyang’anywe wakiwa hawana hata silaha yoyote.

Mheshimiwa Spika, kutokana na matukio ya kikatili kwa wavuvi kuna wengine walijeruhiwa na kuwa walemavu wa kudumu. Mfano mwaka 2020 Ndugu Jeko wa Kata ya Kilangawana alijeruhiwa na risasi mpaka leo ni mlemavu wa mkono na shingo. Wakati huo Ndugu Mwakilima alipigwa risasi mpaka kupoteza maisha na askari wa TAWA anayeitwa Manyama akiwa na askari mwenzake. Pamoja na tukio hilo kuripotiwa Kituo cha Polisi Laela bado hamna hatua zozote zilizochukuliwa na askari huyo yupo bado kazini. Kitendo hiki cha kinyama, kimeleta chuki kubwa sana kati ya wahifadhi na wananchi wa maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, kuanzishwa kwa vibali vya uvuvi; baada ya wavuvi wengi kufa na kuwapo kwa msuguano mkali kati ya wananchi na wahifadhi, TAWA walikuja na mpango wa vibali maalumu kwa kila mvuvi anayetaka kuingia kuvua ndani ya Ziwa Rukwa. Kuanzishwa kwa mfumo wa vibali vilivyotengenezwa na TAWA, badala kuwa suluhu ya tatizo, imekuwa sasa kama nyezo ya kumkomoa mvuvi. Kwa sababu mtindo wa kibali umeleta adha nyingi sana tena za kinyonyaji kama ifuatavyo: -

Kwanza, mvuvi anatakiwa awe na kibali toka TAWA kinachomruhusu kuingia ndani ya ziwa na kuvua kwa miezi sita wanalipa shilingi 15,000. Mvuvi anatakiwa awe analipa kibali cha ngalawa toka TAWA kinachomruhusu kuingia ndani ya ziwa na ngalawa na kuvua kwa miezi sita wanalipa shilingi 15,000.

Pili, mvuvi anatakiwa kulipa kila siku anapoingia ziwani kuvua shilingi 5,000; tatu, mvuvi anatakiwa kulipia ngalawa ya kuvulia kwa kila siku anapoingia ziwani shilingi 2,000; na nne, mvuvi anayetumia boti anatakiwa kulipia engine ya boti kila siku anapoingia ziwani kuvua shilingi 20,000 na boti yenyewe analipia shilingi 2,000.

Mheshimiwa Spika, tano, mnunuzi wa samaki hata kama ananunua samaki mmoja anatakiwa kulipa kila siku anpoingia ziwani kwenda kununua samaki analipa shilingi 4,000; na mwisho akina mama wachakataji kwa maana kuparua samaki nao wanalazimika kulipa kila siku anpoingia ziwani kufanya kibarua hicho analipa shilingi 4,000. Pamoja na ukweli kwamba kipato chao ni cha chini sana kwa kazi hiyo ambapo akipata kiasi kikubwa kwa siku ni shilingi 6,000 na mara nyingine wanaweza wasipate chochote kutokana na upatikanaji wa samaki siku hiyo.
Kwa hiyo, TAWA kwa kipindi cha miezi sita inatoza wastani wa shilingi 4,890,000 ambayo ni sawa na shilingi 815,000 kwa mwezi mmoja ambayo ni fedha nyingi sana kwa mvuvi wa hali ya chini. Wakati huo huo mvuvi ana tozo nyingine kwenye taasisi nyingine za Serikali ambazo anawajibika kulipa kama ifuatavyo; leseni ya mvuvi ya Halmashauri analipa kwa mwaka shilingi 20,000; leseni ya ngalawa ya Halmashauri analipa kwa mwaka shilingi 20,000; na leseni ya TASAC mvuvi analipia ngalawa kwa mwaka shilingi 50,000.

Mheshimiwa Spika, kutokana na tozo kuwa nyingi tena kandamizi kwa wavuvi wamelalamika sana kwenye uongozi wa Uwanda Game Reserve, lakini majibu yao kwamba wao hawana mamlaka yoyote isipokuwa Waziri mwenye dhamana na Wizara hii ya Maliasili na Utalii japo nao wanakiri kuwa tozo hizo ni nyingi mno na kandamizi sana kwa wavuvi ila zipo juu ya uwezo wao.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo yangu kwanza Uwanda Game Reserve ambayo kwa sasa ni ziwa kwa asilimia 80, tunaomba eneo la hifadhi kwenye ziwa liwe mita 500 kama ilivyo kwenye hifadhi zingine zinazopakana na ziwa.

Pili, kipindi tunasubiri kurekebisha kwa mipaka ya hifadhi kama Serikali itaridhia; tozo zile za kila siku kwa mvuvi kuingia ziwani kuvua zipunguzwe walau ziwe hata shilingi 500 na tozo ya ngalawa nayo iwe shilingi 500 kwa kila siku ambapo kwa mwezi mvuvi atalipa jumla ya shilingi 30,000. Hapo tutakuwa tumemsaidia mvuvi kujikwamua kutoka kwenye umaskini. Kwani ilivyo sasa ni kama kumkomoa mvuvi.
Tatu, kipindi tunasubiri kurekebishwa kwa mipaka ya hifadhi kama Serikali itaridhia; tozo zile za kila siku kwa wanunuzi na akina mama wachakataji wa samaki kuingia ziwani kufanya shughuli zao zipunguzwe walau ziwe hata shilingi 500 kwa siku.

Nne, tozo za miezi sita kwa mvuvi kuingia ziwani kuvua zenyewe zibaki; tano, kipindi tunasubiri kurekebisha kwa mipaka ya hifadhi kama Serikali itaridhia hasa kwa wavuvi; tunaomba alama ya mipaka iweke ili kuepusha migongano kati ya wahifadhi na wavuvi na sita, kwenye forodha ya Ilanga Muze inayopakana na Hifadhi ya Lwafi, ziwekwe upya alama zilizoonesha maeneo ya kuvua kulingana na makubaliano ya awali kati ya wavuvi na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga na Mlele Mpimbwe kabla ya TAWA kuja kwani utaratibu wa mwanzo ulikua mzuri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na malalamiko haya kujirudia mara nyingi na wavuvi kuathiriwa sana tunaomba zoezi la kuwakamata wavuvi wakiwa ziwani kusubiri mpaka hapo alama za utambuzi zitakapowekwa. Kwani wavuvi wanashindwa kujua mipaka ya eneo la hifadhi na eneo lisilo hifadhi. Wavuvi waliahidiwa kwa muda mrefu kuwekewa alama mpaka sasa hamna kinachoendelea.

Mheshimiwa Spika, wavuvi wanaokamatwa hasa kwenye forodha ya Ilanga iliyopo Halmashauri ya Sumbawanga, wasipelekwe Halmashaurui ya Mlele Mkoa wa Katavi kwani ni mbali sana. Hii inapelekea wao kukosa haki zao kwa sababu wanakuwa hawana hata mtu wa kuwadhamini na inapokuwa kesi imeenda mahakamani inakuwa shida kupata dhamana.

Mheshimiwa Spika, tunaomba kuwepo na vikao au mkutano ya pamoja kati ya askari wako wanapoingia ili kuweka mahusiano mazuri kati ya wavuvi na askari wanyama pori. Pia tunaomba jambo lolote linalowahusu wavuvi au taarifa yoyote ile ya wavuvi itolewe kupitia vyama vyao, Wenyeviti wa Makambini siyo mtu binafsi ili kuondoa makanganyiko na habari za uzushi kusambaa.

Kuhusu taarifa ya Mawaziri Wanane wanaotatua migogoro itoke mapema ili wananchi waweze kuendelea na shughuli zao. Kwani kwenye Jimbo langu la Kwela tuna vijiji 16 wenye mgogoro na hifadhi ya Uwanda na mwaka huu ndio hali ni mbaya kabisa, wananchi wameshindwa hata kufanya shughuli za kilimo kutokana na mgogoro huo, kwani walizuiliwa na wahifadhi kulima hata maeneo ambayo wamekuwa wanalima miaka ya yote ya nyuma. Sababu ya wahifadhi kwa wananchi ni kwamba wasubiri ripoti ya Mawaziri Wanane ambayo waliahidiwa ingetoka mwaka jana mwezi wa nane, lakini mpaka leo kimya.

Mheshimiwa Spika, kama itakupendeza Mheshimiwa Waziri upange ziara uje kujionea mwenyewe hali halisi juu ya mgogoro huu ulioathiri wakulima, wavuvi na wafugaji kwa kipindi kirefu sana. Kwa mfano ndani ya Jimbo langu la Kwela zaidi ya kata nane zipo kwenye mgogoro huu, hii ni hatari. Alikuja mwaka jana Katibu Mkuu wa CCM Taifa na Naibu Waziri wako waliona hali ya malalamiko kwa wananchi yalivyokuwa makubwa.

Mheshimiwa Spika, wahifadhi waache kutumia nguvu kubwa kupita kiasi wanapokabiliana na wananchi hasa wavuvi, kwani vifo vilivyotokea na watu kupata ulemavu vimezidisha chuki kati wananchi na Serikali. Hatua kali zichukuliwe hasa kwa askari wanaofanya vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu, mfano yule anayetuhumiwa kufanya mauaji ya mvuvi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika hoja iliyo mezani, hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza nichukuwe nafasi hii kuipongeza Serikali; mimi binafsi katika jimbo langu kwa mara ya kwanza tumeweza kupata fedha nyingi za maendeleo ambazo zinafikia takribani bilioni tisa. Ni rekodi kubwa, na mimi pongezi zangu za dhati za wanakwela zimfikie Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo nitoe tu ahadi kama Mbunge na Baraza langu la Madiwani tutasimama kidete kuwahakikisha fedha hizi zinafanya kazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili naomba nitoe mchango wangu, na nitaanza kuchangia katika sekta ya bandari. Bandari ni key driver ya uchumi ndani ya nchi. Sisi kama Tanzania tuna bahati, upande wa Mashariki wa nchi tuna Bahari ya Hindi ambapo tuna bandari, upande wa Magharibi ya nchi tuna Ziwa Tanganyika ambako ndiko kunapatikana Mikoa ya Kigoma, Katavi na Rukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kumekuwa na sintofahamu ya muda mrefu. Hapa ameongea ndugu yangu Mheshimiwa Kandege, kwamba kati ya mikoa inayotajwatajwa kuwa na umaskini na hali duni ya maisha ni mikoa ya Rukwa, Katavi Kigoma na sisi tuna Ziwa Tanganyika ambalo tunapakana na nchi ambazo zina fursa ya kufanya biashara na nchi yetu kupitia ile mikoa mitatu. Kule tuna Burundi, DRC na Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe tutaarifa. Juzi tu hapa kuna ugunduzi umefanyika wa copper ndani ya nchi ya DRC kule Katanga kuna deposit ya copper ambayo wanaweza wakafanya uchimbaji kwa miaka 100 ijayo. Sasa fursa pekee ambayo tunayo, wao wanategemea kusafirisha raw materials katika extraction ile ya copper ambayo ni sulphur ambayo wanaipitishia Bandari ya Dar es salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa taarifa tu ile biashara ya sulphur
ambayo wanapitisha Bandari ya Dar es salaam imeweza ku-trigger namba za mapato ndani ya mapato ndani ya Bandari ya Dar es salaam. Yale mapato waliyokuwa wanaweza kuyafanya kwa mwaka mzima kwa mwaka huu kwa mara ya kwanza wataweza kufikia ndani ya kota mbili kwa maana ya miezi sita. Ni achievement kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa shida ambayo imekuwa ni kikwazo biashara hii tusifanye vizuri na DRC ni mzunguko. Wakichukuwa mzigo huo Bandari ya Dar es salaam wanalazimika wapitishe Zambia ndipo waende Lubumbashi. Mzunguko mrefu sana ilhali sisi tuna short cut ya kupitia either Kasanga, Kalema ama Kigoma kwenda upande wa pili wa DRC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi mpaka tunavyoongea mwaka wa tatu tuna bajeti kwamba tunanunua meli. Ziwa Tanganyika hatuna meli, tangu Liemba iondoke kwenye matengenezo, tangu MV Mwongozo iondoke hatuna meli. Sasa, tutaweza ku-utilize opportunity hii ya DRC, iliyokuja, kwa namna gani? Wataanza kufikiria kutukimbia, wataenda Bandari ya Walvis Namibia au Beila kule Mozambique au wataamua kwenda Durban South Afrika. Sasa naomba, Mheshimiwa Waziri Mkuu tumewekeza kwenye Bandari zetu za Kasanga, Kalema pamoja na Bandari ya Kabwe. Sasa zile bandari kazi yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo hili ambalo hatuwezi pia pamoja kwamba bandari zitakamilika, upande wa pili wa kule DRC miundombinu ya barabara ni shida. Kutoka pale Moba upande wa pili kwenda kufika Lubumbashi ni kilometa 700, kilometa hizo hazipitiki. Kwa hiyo kama nchi lazima pia tufanye mazungumzo ya pamoja na nchi ya DRC kama wenzetu wa Uganda walivyofanya, tukaingia hata katika ubia wa kutengeneza barabara ili tuwende ku-utilise opportunity iliyoko ndani ya nchi ya DRC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali, mikoa yetu hii itafunguka; leo hii bodi ya mazao mchanganyiko mmeanzisha ghala kule Lubumbashi, mahindi yetu yataendaje? Ina maana tutapitisha Zambia ndipo tukauze kwenye soko la DRC? Haiwezekani, hatuwezi tukategemea boti za watu binafsi kama nchi kusafirisha mizigo yetu ambayo inaenda ku-trigger uchumi wa mikoa mitatu kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tena, Mheshimiwa Waziri Mkuu, jambo ambalo mimi nimekuwa nikipata shida wakati huu, kumekuwa misconception ya kuchanganya kana kwamba Mkoa wa Rukwa na Katavi ni mkoa mmoja. Tayari mikoa hii imeshakuwa tofauti. Katavi wanajitegemea na Rukwa inajitegemea. Leo hii kuna mradi huu ambao tumepata fund kutoka kwenye European union agri-connectivity kwa ajili kutengeneza miundombinu ya barabara ku-support productivity kwenye kilimo. Mikoa yote ya Nyanda za Juu Kusini ipo, ikiwemo Katavi, lakini Rukwa wameturuka, sisi Wana-Rukwa tuna shida gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo niombe sana, tunapokuwa tunaangalia kwa upana namna ya kuweza, leo hii tumeongelea hapa, nimemsikia ndugu yangu hapa anaongelea habari ya uwanja wa ndege wa Sumbawanga. Ule uwanja wa ndege wa Sumbawanga ni miaka sita sasa, kila bajeti ipo; na nilivyokuwa namwona Mheshimiwa Waziri anajibu hapa nikatikisa kichwa, kwamba na mwaka huu wananchi tunaenda kuwaambia kwamba imo kwenye bajeti tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwaambie kama inashindikana mwaka huu kutekeleza ni bora tuiondoe kwenye bajeti ili tujuwe kwamba mwaka huu hatuna uwanja wa Sumbawanga. Niendelee kusihi sana asubuhi tulikuwa na jambo la mbolea limeongelewa na Mheshimiwa Waziri amejibu sana. Kama hatutafufua kampuni yetu ya mbolea Tanzania TFC tusitegemee kwamba suala la mbolea tutapata suluhu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongea habari ya ruzuku, ni sawa, lakini mnapowapa nguvu private operator kwenye suala la mbolea ambayo ni sensitive kwa usalama wa chakula cha nchi ni shida. Hili shirika letu ambalo liko taabani tangia mwaka 2014 limekufa; na hili shirika si la juzi, limeanzishwa mwaka 1968 kwa dhumuni la kusaidia usalama wa upatikanaji wa mbolea ndani ya nchi; lakini tulilitwishwa mzigo wa madeni limekufa halipo kabisa. Kwa hiyo inatakiwa Serikali tuchukuwe hatua ya haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tumeahidi kwenda kuweka ruzuku ili tupate mbalea nchini, nawasihi sana tuifufue Kampuni ya Mbolea Tanzania ili itusadie Watanzania wakulima maskini ambapo mwaka huu mbolea ni kilio cha nchi. Ukifika kule kwetu tumeenda mpaka 140,000 kwa mfuko mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa nafasi hii. Haya yalikuwa ya kwanga niliyotaka kuchangia katika Ofisi ya Waziri Mkuu ahsante sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa fursa hii na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye taarifa zilizowasilishwa hapa. Kwanza kabisa nianze kwa kuunga mkono hoja kwa Kamati zote tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitaanza kwanza ku-recall katika Bunge la Bajeti ndani ya Bunge hili, tulipisha fedha nyingi zilizoenda kwenye Wizara ya kilimo ambayo inaenda takribani Bilioni 954. Kati ya fedha hizo asilimia 35 inaenda kwenye sekta ya umwagiliaji, tunatamani na Wabunge tunaamini kwamba fedha hizo zilizopitishwa zinaenda kuleta mabadiliko makubwa kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitarudi nyuma mwaka 2018/2019 CAG alifanya ukaguzi kwenye miradi Tisa ya umwagiliaji, ambayo ilifanyika chini ya Wizara ya Kilimo, Wizara ya Kilimo ilikuwa inasimamia miradi miwili na miradi Saba ilikuwa chini ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji. Alikutana na mambo mengi ya ajabu na hii itupe fundisho kwamba tunapoenda kutekeleza miradi ya umwagiliaji tuliopewa pesa Bilioni zaidi ya 300 tupate somo kwa miradi hii ambayo imefanyika na imepelekea Taifa hili hasara kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na miradi ile miwili ule wa Msolwa pamoja na Kingali iliyofanyika chini ya Wizara ya Kilimo. Ile miradi ilikuwa na mambo mengi ya ajabu. Kwanza Msanifu aliyepewa kusanifu alipewa kazi hajaona site, ni mtu aliyepewa kazi akiwa ofisini, mradi wa shilingi milioni 835 na baadae akaleta ripoti, ripoti ile alipowaletea wataalam Wizarani hawakufanya uhakiki, moja kwa moja wakaingia field na baadae akawaletea yeye binafsi kwa kufanya kazi ile variation ya karibia asilimia 58. Kwa hiyo, kutoksa milioni 835 alienda kulipwa zaidi ya bilioni moja na milioni mia tatu. Kwa hiyo, ikawa variation ya asilimi 56 na hiyo ni kinyume na Sheria ya Manunuzi iko-very clear.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Manunuzi ili uweze kufanya variation ni plus fifteen or minus fifteen kwa maana fifteen percent kama unaongeza na kama unapunguza ni fifteen percent. Nje ya hapo scope hiyo haipo rudia upya tangaza tenda upya maana yake ni kitu kizima. Kwa hiyo, watu hawa wakafanya maksudi wakaingiza Serikali hasara kubwa!

Mheshimiwa Naibu Spika, hawakuishia hapo huyu mtaalam mwelekezi hakufanyiwa due diligence, katika application yake aliambatanisha CV za wataalam lakini kumbe wale wataalam ilikuwa ni gelesha, walioenda kufanya kazi actual field hawakuwa wale walio-submit zile CV. Kwa hiyo ilikuwa ni kuwa-fix wale watu wa evaluation wamu- award tender wakishamu-award wanaoenda ku-perform ile contract kwenye field ni watu wengine ambao ni makanjanja, haya mambo yamefanyika kwenye miradi ya umwagiliaji ambayo pesa ile pia ilikuwa ni mkopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo inakopwa kuja kufanya kazi za maendeleo, kuna watu wajanja wanajiita wataalam wako huko Wizarani. Juzi nimekuona Mheshimiwa Bashe uko huko Ruvuma tayari wameshaanza kukuchezea, tayari Mkandarasi mwaka huu fedha hizi ameenda kufanya madudu Ruvuma na ume-terminate contract! Hiyo ni postmortem hatutakiwi kufanya postmortem, kuanzia stage ya kwanza tunapoanza initial procurement proceedings lazima tuhakikishe kwamba kuna compliance. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutaenda kwa staili hii ya kufanya postmortem ya ku-terminate contract tutaliingiza Taifa hili hasara kubwa sana. Huyu mtu hajafanyiwa due diligence na average ya mikataba yote imechukua muda mrefu sana zaidi ya siku 450 amezidisha kwenye ku-implement huu mradi, leo hii tumepitisha kwenye Bunge hili tuna miezi 18, sitarajii baada ya miezi 18 tuje tuanze kufanya the same post-mortem ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, huku ndiyo tunaona Watanzania wote kwenye kilimo kwenye umwagiliaji hawakuishia hapo wameendelea miradi mingine mitatu waka-award contract walivyo-award contact Tume hii ya Taifa ya umwagiliaji baadae wakasaini mkataba na Wakandarasi hawa watatu, walivyosaini mtakaba kesho yake wasema hatuna fedha tuna-terminate hizi contract. Sasa kuna litigation issue, legal status ya mambo haya iko wapi? Mtapelekwa Mahakamani kama Wizara! Kama mlijua hamna fedha nani aliwatuma mkatangaze tenda na Sheria ya Manunuzi iko very clear. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hautakiwa ku-initiate procurement proceedings kama hamna availability of budget, full stop. Sasa mlienda sijui wapi. Baada ya muda mfupi wakatangaza tena upya, kuna Tender Board zinakaa hapo ni cost za walipakodi tena Wizara maskini kama Wizara ya Kilimo ya watu ambao ni wanyonge, mnakaa Tender Board mna-award mnasaini mikataba na mikataba kwa sababu ni mikubwa ni ya Mabilioni inaenda mpaka kwa AG. AG naye kule anaenda kufanya vetting inarudi mnakuja pale kwamba sisi tume tume-cancel kesho tunatangaza upya tenda! Taifa hili linachezewa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawakuishia hapo, baada ya ku-award wameendelea na michezo hiyo wakawa-award tena Wakandarasi wengine mikataba mitatu iko hapa, walivyowa-award wale watu hawaku-perform wakashindwa, Tume ikasema kwamba basi jamani, safi ninyi ni Watanzania meshindwa tupeni, wakaenda kufanya kwa force account wakatumia tena fedha zilezile za Tume ya Umwagiliaji ku- implement miradi ile ile kwa force account wakati kuna Mkandarasi walimpa. Hatujawahi kusikia kwamba Mkandarasi alipelekwa Mahakamani kwa ajili ya liquidated damages, hatujawahi kuona kwamba kuna hatua zozote kali zimechukuliwa, business as usual, maisha yanaendelea tumepewa Bilioni 300, na nampa alert Mheshimiwa Bashe hatutaki tena baadae story kama hizi. (Makofi)

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango mzuri anaoendelea nao kuzungumza mzungumzaji, nilitaka nimpe tu taarifa kwamba changamoto unayoiona sasa hiyo kwenye Tume ya Umwagiliaji Fungu 05, tayari kwenye fedha za ECF nilizokuwa nazizungumza wamepewa bilioni 215, sasa changamoto ikija hiyo sasa sijui kama tutaendelea kupewa zile Awamu Sita zilizobakia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hiyo tu taarifa niliyokuwa nampa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Deus.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa. Leo sina mambo mengi nilikuwa mime- focus tu kwenye Tume ya Umwagiliaji na rafiki yangu Mheshimiwa Bashe Waziri wa Kilimo, umenipa mradi mkubwa nashukuru lakini jambo hili tusimame pamoja tukaisimamie hii Tume ya Umwagiliaji. Nakuamini sana, nakuomba sana pesa zote wanachezea huku tunapiga kelele sawa, mmefanya reshuffle mmemuweka MD mpya na nini. Tunaomba muende mpaka chini, wataalam Maafisa Manunuzi wadogo mnawaacha... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Kwanza nimpongeze Waziri na Naibu wake kwa namna walivyoanza kwenye Wizara hii wameanza kwa utulivu na usikivu mkubwa, wakienda kwa spirit hii tutakwenda mahali pazuri.

Mheshimiwa Spika, leo nina mambo mawili; moja ni la jimboni kwangu; Nimekufuata Mheshimiwa Waziri mara nyingi. Mwaka 2019 aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, alipotembelea jimboni kwangu katika Mji Mdogo wa Laela akiwepo na Waziri wake wa Mambo ya Ndani wakati huo Kangi Lugola, walitoa ahadi ya kuwarejeshea wananchi ekari 495 ambao ni mgogoro na Gereza la Moro kule Sumbawanga.

Mheshimiwa Spika, agizo hilo ni mwaka wa tatu na nimeuliza swali hapa Bungeni utekelezaji wake umekuwa ni sifuri, nimemfuata na wakati huo mtangulizi wake kaka yangu Simbachawene, nilimwambia jambo lile lina shida kubwa kwa sababu gereza mipaka yake imeingilia mipaka ya kijiji, ndiyo maana viongozi waliotangulia walitumia busara angalau kuwapa wananchi wale wa Msanda Muungano ekari 495. Nashindwa kujua tatizo liko wapi na kwa nini wanapata kigugumizi kufanya jambo hilo. Nmwombe kwa usikivu huo huo niliousema na namna ambavyo anafanya mambo yake kwa wakati mfupi huu, naomba jambo hilo tukali-close ili tuachane na mgogoro na wale wananchi.

Mheshimiwa Spika, Wizara wana mpango wa kwenda kuwekeza kwenye gereza lile, kama hawata-solve mgogoro na wale wananchi, impact yake itakuwa mbaya sana. Namwomba sana na nilikusudia kushika shilingi kwa jambo hili ila amenihakikishia kwamba baada ya Bunge tutakwenda kule ku-address lile tatizo.

Mheshimiwa Spika, jambo langu la pili ni suala la Jeshi la Polisi. Mfuko wa Tozo na Tuzo. Huu Mfuko na mara nyingi Naibu Waziri amekua ukijibu swali ambapo Waheshimiwa Wabunge wanaomba Vituo vya Polisi anasema tutajenga kwa kupitia Mfuko wa Tozo na Tuzo. Kinyume kabisa na Sheria ya Fedha Public Finance Act. Mfuko ulivyo, una takribani miaka 10 sasa; kwa jinsi ulivyotengenezwa hata kwenye Fungu Na. 28 la Jeshi la Polisi leo hakuna fedha hiyo ilivyooneshwa kwamba itapatikana, lakini three years consecutive Jeshi la Polisi limeweza kukusanya zaidi ya bilioni 32 toka kwenye Mfuko huo na mwaka jana tu wametumia zaidi ya bilioni sita bila ya kupitishwa na kuidhinishwa na Bunge. Hatuwezi tukapata tija ile tunayoitaka kwa sababu gani? Haya maendeleo ujenzi sijui wa Vituo vya Polisi, nyumba za polisi, hautakwenda kwa usawa kwa sababu itategemea na nani aliyepo kwenye menejimenti ya Jeshi la Polisi na ana utashi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri, tungeweza kuivuruga hii bajeti, lakini italeta shida. Naomba CAG akakague huo Mfuko miaka 10 haujawahi kukaguliwa, haujawahi kufanyiwa reconciliation na fedha zinaingia na kutoka; ukienda kule Hazina wanasema hizi fedha ni za Jeshi la Polisi. Ukija Jeshi la Polisi wanakwambia zipo Hazina, kwa hiyo CAG ameshindwa kufanya hata auditing miaka yote hii. Mbaya zaidi huu Mfuko ni fedha zinazokusanywa kutokana na huduma za ulinzi, Benki na kwenye migodi. Kumekuwa malipo ambayo client anafanya moja kwa moja kwa Polisi yaani anawalipa anakwenda kulinda Polisi Benki analipwa Sh.10,000 wanakuja ku-deduct kwenye mkataba, jambo ambalo halipo kabisa kwenye finance. Public Finance Act inaeleza, ilibidi zile fedha wazikusanye, ziingie kwenye hiyo account, baadaye sasa Jeshi la Polisi ndiyo wawalipe wale askari kama ni risk allowance kuliko inavyofanyika sasa hivi ambayo client mwenyewe anasema haya nakupa shilingi 10,000 saini hapa, tutakatana kwenye mkataba; mambo ambayo ni yanafanyika locally, haitakiwi na nashangaa huko Jeshi kuna Wataalam wa finance? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwanza tukafanye hii audit; na kuna miradi mingi imekwama, mfano, tumetembelea juzi Ikungi, tumekuta jengo la Jeshi la Polisi la zaidi ya bilioni tu lilijengwa miaka saba iliyopita kutokana na Mfuko huo wa Tozo na Tuzo. Badaye viongozi wa wakati ule wameondoka, wamekuja wapya, wakatelekeza fedha za wananchi.

Mheshimiwa Spika, Jimboni kwangu, sijawahi pata hata senti moja hii fedha inayotokana na Tozo na Tuzo. Vituo vyangu vya Polisi karibu 11, tumejenga kwa nguvu za wananchi ndani ya Jimbo la Kwela kwenye Kata 28. Sasa tukileta hapa Bungeni tutakuwa na Mandate ya kui-discuss hii fedha, tuone kwanza upatikanaji wake na mgawanyo wake ukoje ili kila Mbunge aliyekuwepo hapa ajue huu Mfuko wa Tozo na Tuzo huu unamgusa vipi kwenye jimbo lake. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mawazo yangu na mchango wangu kwenye Wizara hii muhimu sana, Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayofanya, lakini culture waliyonayo, kwa maana hierarchy ya Wizara yao yote ni wasikivu, Katibu Mkuu, Meneja wangu wa Mkoa ndugu yangu Boaz, unafanya kazi nzuri na Meneja wa SUWASA ndugu yangu Nzoa na Meneja wangu wa Wilaya, Maganga. Kwa kweli kazi yao ni nzuri, wanatupa ushirikiano mzuri kiasi kwamba, tunafurahia sana huduma katika Wizara yako hii ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaanza kwa shukrani kubwa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwanza kwa mile stone tuliyopiga kwenye miradi ya maji. Kwa muda mfupi nimeingia kama Mbunge nimeweza kushuhudia maajabu. Ajabu ya kwanza ambalo nitalisema kwako na kwa moyo mkunjufu ni mradi ule wa Ziwa Dogo la Kwela ambako sasahivi mko kwenye final stage ya kusaini mkataba wa bilioni tano. Utahudumia Kata za Kalambanzite, Lusaka, Laela, Nyangalua na Mnokola. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri tumepata fedha hizi bilioni tano ni za mwanzo tu, lakini umuhimu wa mradu huu uta-justify na investment hii kwa sababu return ya hii investment ni pale tutakapofikisha maji haya katika Mji Mdogo wa Laela, Mnokola na Miandalua. Sasabu hii ya kusema ni nini, tuna chanzo kile kimeishiwa nguvu, ambacho Serikali iliwekeza bilioni 2.6 pale kwenye Mji Mdogo wa Laela umefika mara nyingi na badaye kukatokea mgogoro mkubwa umechukua miaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pale kuna shida nyingine. Ule mradi mwanzo ulikuwa unatumia system ya solar; mliwekeza kama shilingi milioni mia moja na kidogo kwa ajili ya kununua solar. Solar ziko pale ziko redundant na mara nyingine sisi tunapata shida kupata maji kwenye Mji Mdogo wa Laela kwa sababu moja tu kwamba, umeme tunaotegemea ni wa Zambia. Wakati mwingine inapita hadi wiki mbili hatujapata umeme kwa hiyo, tunakuwa hatuwezi kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikuombe kwa kauli yao Mheshimiwa Waziri turudi, zile solar zinakaa pale zitakuwa obsolete. Tuzitumie ili zitusaidie ili zitusaidie pale tunapopata shida ya umeme zisaidie ku-pump maji ili wananchi wa Mji Mdogo wa Laela waweze kupata maji. Lakini chanzo cha Kwela ndio kitaenda kumaliza matatizo ya kudumu kabisa kwa sababu ukifika mwezi wa saba na wa nane maji yanakuwa ndoo moja shingi elfu moja mpaka elfu mbili katika Mji Mdogo wa Laela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili nishukuru sana Serikali kwa mradi mkubwa wa kihistoria utakaotekelezwa ambao unaitwa Kaoze Group kule Bonde la Ziwa Rukwa. Mradi ule utaleta manufaa makubwa. Nashukuru mmetangaza kuanza na Kata ya Kaoze kwa bilioni moja na milioni 500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimuombe Waziri, kwa mradi ule wa mamu, ule wa Marekani, ambao umekuja, muweze kupeleka mpaka vijiji vingine 13, kwa maana ya Kata za Kipeta na Kilangawani, ili wananchi wale ambao tangu ulimwengu huu kuumbwa hawajawahi kupata maji safi na salama na hawajawahi kuona maji kutoka kwenye bomba. Nikuombe ndugu yangu Waziri umekuwa ukinipa ushirikiano mzuri na Naibu wako, twendeni tukafanye jambo kubwa kwenye mradi huu wa Kaoze Group ili wale wananchi waweze kuandika historia kwamba, alipita Mheshimiwa Aweso, kama Waziri, alitufanyia miujiza mikubwa ambayo hawajawahi huona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee kuna ule mradi wa Bwawa la Ikozi, unalifahamu sana una miana zaidi ya minne bilioni 1.5 tumewekeza pale. Shida iliyopo pale kuna mambo mawili; kwanza kuna mgogoro ule na wale wananchi waliotoa yale mashamba. Nikuombe Waziri kuna mambo waeleweshwe tu wale wananchi, miaka minne hawajaeleweshwa kama kuna fidia au hakuna. Ni kuwaweka tu wapate clarity ya mradi ule utakavyokuwa, wakishajua hawana shida, maana wameshindwa kupata jibu kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, twendeni tukawaambie ili pesa ulizoleta hizi karibuni tumesaini mkataba wa bilioni mbili wakaone faida ya hela ya mama bilioni mbili, sio ikatokea bilioni mbili imewekezwa pale muda mfupi tuanze kupata sabotage ya wananchi kwa sababu wana complain kwamba kuna mgogoro kwenye eneo lile la Ikoze. Najua ni jambo dogo kwako utaenda kuli-address ndani ya muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nishukuru pia kwa mradi mkubwa sana ambao unaenda kuhudumia Mkunda Group, Kijiji cha Kaengesa, Kianda pamoja na Kijiji cha Itela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe jambo moja. Kuna vijiji viwili katika mradi huu vimesahaulika na viko njiani; Kijiji cha Katonto na Kijiji cha Kazi. Naomba tunapofanya huu mradi ambao tayari nao umesaini mkataba viwe included ili waweze kao kunufaika nah ii pesa bilioni moja na milioni 700 ambayo mama amewaletea wananchi wa Kata ya Lyangalile na wa Kata ya Kaengesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa namna kubwa kabisa na Wabunge wenzangu wa Kigoma, Katavi, Rukwa na Songwe wameongea. Mradi ambao utakuwa tiba ya kudumu ya tatizo la maji katika mikoa hii minne ni mradi kutoka Ziwa Tanganyika. Tuombe sana; investment ni kubwa tunakubali, lakini return ya investment hiyo na economies ya scale ambayo itapatikana kulingana na huu mradi itaenda kumaliza tatizo hili na hii miradi midogo ambayo life span yake ni miaka 20 tutaachananayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana pia kwa CSR uliyotoa pale kizungu ndani ya Kata yangu Muze, nakushukuru. Umekuwa kati ya Mawaziri waaminifu; ukipita ukaahidi jambo unatenda, maana kuna jamaa zangu walipita jimboni kwangu wakaahidi CSR miaka mitano, wengine mpaka wameondoka kwenye uwaziri nimesahau kabisa, ila wewe uliahidi ndani ya mwezi mmoja na muda mfupi ukaleta ile CSR. Nikupongeze ndugu yangu Mheshimiwa Aweso kazi yako imetukuka hakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho nishukuru pia kwa mradi ule unaoendelea wa Uviko pale Mwadui, Kata ya Mwadui, lakini pesa tuliyotenga kwa ajili ya Kata ya Kasekela. Halikadhalika Ilemba pale kwa mara ya kwanza nao watapata maji ya kutosheleza. Nikupongeze sana Waziri, kwa kweli mimi hayo niliyoyasema ndio nakuomba sana, Lake Tanganyika ndicho kilio chetu, ndio suluhu ya matatizo katika mikoa yetu hiyo minne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye Bajeti hii ya Ofisi ya Rais TAMISEMI. Kwanza kabisa nikupongeze Mheshimiwa Waziri na timu yako hapa ya wachapakazi na mnafanya kazi nzuri katika wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii ndani ya Bunge hili kutoa pole kwa wananchi wangu wa Jimbo la Kwela katika Kijiji cha Talanda Kata ya Mileka kwa maafa yaliyotokea, ambapo mafuriko makubwa yamesababisha vifo vya watu saba na zaidi ya kaya 20 zimekosa makazi. Nishukuru Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ametuahidi atatuma timu na dada yangu Jenista uko hapa mtusaidie kwenda kutoa msaada wa kibinadamu kwenye ofisi yako kwa maana ya Kitengo cha Maafa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa aliyoifanya ndani ya Jimbo la Kwela. Nina mirad mikubwa mingi ambayo nikianza kusema hapa nitatumia muda mrefu sana lakini nina forum ambayo tutaendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina mambo machache ya kijimbo na baadaye nitaongea mambo ya jumla ya kitaifa. Jambo la kwanza ambalo nakuja kwenu ni ombi. Katika Jimbo langu la Kwela Mji Mdogo wa Lahela hatuna hospitali kabisa. Tuna jengo ambalo ni Mji wa Makao Makuu ya Wilaya ni mji ambao ndio center kubwa katika ndani ya Jimbo la Kwela lakini hatuna hospitali. Kwa maana ya kwamba tuna kituo ambacho kinamilikiwa na Kanisa Katoliki, wametupangisha pale kwa muda wa miaka 40 na hatuna umiliki wowote kama Serikali. Sasa makao makuu ya wilaya kukosa hospitali na huduma pale kimezidiwa kwa sababu population imekuwa kubwa. Niwaombe, ombi hili nimelileta mara nyingi wizarani mnalijua, naomba tulipe kipaumbele ili kuipa hadhi makao Makuu ya Wilaya, Halmashauri yetu ya Sumbawanga ambayo ni mji mdogo wa Lahela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la pili kwenu ndugu zangu Mheshimiwa Waziri naamini ni wasikivu, bajeti yetu ya TARURA ipo inafanya kazi yake nashukuru imeongezeka na hili nampa sifa Mheshimiwa Rais. Lakini kuna barabara maalum, kuna barabara ya kutoka Chombe, Kiandaigonda kwenda mpaka Kaozi ni kilomita 18.8. Barabara hii ni korofi na na barabara muhimu ya kimkakati katika uchumi wa kukuza na kupata mapato ndani ya halmashauri yangu. Ombi langu kwenu, naombeni mfanye hima ili mtusaidie na sisi Halmashauri ya Sumbawanga tuweze kukusanya mapato na tufikie malengo yetu ndani ya halmashauri; mtupatie fedha za dharura kutengeneza barabara hii muhimu. Najua jambo hili liko ndani ya uwezo wenu bajeti ya kwaisa ya TARURA haitoshi muifanyie udharura wake tuweze kuwasaidia wananchi wangu kama hivyo nilivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine muhimu ambalo nawaletea leo ni maboma ya zahanati. Wananchi wangu wamejitahidi, ndani ya vijiji 16 wamejenga zahanati ambazo zimefikia hatua ya mwisho kiasi kwamba tukiwapa fedha kidogo zahanati zile zinaenda kufanya kazi. Kuna Kamsamba, Mtetevu, Tapewa, Kazi, kuna zahanati nyingine ya Mtapenda, zahanati ya Mumba, Zahanati ya Lilolyambula, Zahanati ya Kawila, Zahanati ya Ilambo; ziko zahanati 16 kwa sababu ya muda nitawaletea mzione hapa. Nawaombeni hizi zahanati zinahitaji kupelekewa fedha kidogo zahanati zile zinaanza kufanya kazi na wananchi watapata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo vituo vya afya. Wananchi wangu wa Kata ya Ilemba, wananchi wangu wa Kata ya Mwive wamepambana wamejenga, wamejitolea zaidi ya miaka 10 kujenga vituo vya afya lakini wamefika mahali nguvu imeisha wanahitaji msaada wa Serikali. Nilishaleta maombi haya hapo wizarani nimesema mara nyingi ndani ya Bunge hili niwaombe sasa na sisi tuweze kufurahia neema ili wananchi wa Ilemba, wananchi wa Mwive wafurahie kupata vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni uhaba wa watumishi. Na hili naomba mnisikilize Mheshimiwa Waziri. Pale mnawapa ajira zinatoka vijana wanaripoti vizuri mnawaleta Sumbawanga. Wakishafika Mkoa wa Rukwa wanaanza kuomba uhamisho na uhamisho huo mnatoa mara moja bila kuzingatia hata kwamba wanatakiwa wakae hata miaka mitano kwa mujibu wa taratibu. Kwa hiyo pale imekuwa ni kama sehemu ya kupatia cheque number. Mtu anachukua cheque number anaondoka anaendelea na maisha mengine. Tumepelekea uhaba wa watumishi ambapo kada ya ualimu tu ina upungufu wa walimu 1187, kada ya afya 867. Hali ni mbaya, tumeshindwa, kuna baadhi ya shule hakuna, nina shule 19 hazina hata mwalimu mmoja wa kike nikuombe sana ni hali ya hatari tunaongelea mambo ya unyanyasi wa kijinsia. Halafu shule nzima hakuna hata mwalimu mmoja wa kike, shule 19, hii ni disaster. Tutakuta mama na mwana wanakuja kulaumiwa mimba za utotoni, ubakaji na mambo mengine mabaya yaliyosemwa ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri haya muyachukue na kwenda kunisaidia tupate ajira hizi mpya zitakapotoka muwape kipaumbele Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la nne ambalo ni muhimu nataka niongelee mambo ya usimamizi madhubuti wa fedha tunazopeleka kwenye miradi. Kuna jambo ambalo ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais ndani ya mkoa wetu tunaenda kupata mradi mkubwa kwenye Manispa yetu ya Sumbawanga Jimbo la Mheshimiwa Aeshi, bilioni 27 zinaenda kujenga barabara na kwenda kujenga soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nitoe tahadhari, tuko kwenye mchakato wa manunuzi sasa hivi, kuna mambo tumeyaona sehemu nyngine, hayafurahishi na yanatia dosari Ofisi ya Rais TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri dada yangu wewe ni mchapakazi, tulifanya ziara pale Dar es Salaam kwenye mradi wa DMDP ambao ulikuwa ni Dola za Kimarekani milioni 330, tumekutana na mambo ya ajabu sana. Tulipokutana pale Ofisi Ndogo ya Bunge tukiwa na timu yako ya Wizara kila mtu ameshika tama anasikitika. Vifurushi vyote, package 19 za miradi ile kuna ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha. Nakupa tu mfano ili mpate picha kwamba miradi hii ya TaCTIC ambayo inaenda kufanyika nchi nzima mmejipangaje, mmejiandaa kuifanya miradi hii au tui-suspend kwa kuwa ubadhirifu unakuwa mkubwa na unakatisha tamaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano stendi ile ya Buza mkandarasi walimchelewesha kutofanya kazi kwa siku 289. Hawajamwambia chochote, wako kimya watalamu wako. Baada ya hapo akawaletea madai ya milioni 488 kwamba mmenichelewesha wakalipa bila wasiwasi wowote. Mkandarasi huyo huyo akafanya kazi akamaliza, baadaye wakamchelewesha malipo, alivyoleta certificate wakachelewesha kwa zaidi ya siku 100 akaleta riba ya milioni 879, hasara bilioni moja na kidogo mmeisababishia hasara Serikali. mimi ninalia zahanati 16 kuna mabilioni huku yanaliwa kirahisi tu ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haitoshi, jambo la kusikitisha kabisa, certificate mpaka leo ninavyoongea, ni jambo tumeliona wiki mbili zilizopita nendeni mka-verify; inawezekanaje mtu analipwa certificate kabla hajamaliza kazi? Kuna miradi iko asilimia 68, asilimia 79, asilimia 80 wameshalipa certificate zote na wengine wako site walishalipwa hela zao, akiamua anaweza akaondoka zake hamna cha kumfanya kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuko makini, kila mtu anajifanyia jambo anavyotaka. Niwaombe sana mama anahangaika kutafuta fedha ukiukwaji wa taratibu za manunuzi umekidhiri kwenye miradi hii. Tumekuta pale kuna variation mpaka ya asilimia 125, yaani mradi ni ya milioni 720 mtu ameenda kufanya variation wakati imekuwa bilioni 2.3 nashangaa haya mambo yanafanyikaje? Kwa hiyo ukienda kupitia package ili upate somo zuri Mheshimiwa Waziri kapitie package 19 zote za miradi ule wa DMDP utakuta kuna madudu. Uki- sum-up ile cost wewe mwenyewe kichwa kitakuuma utaenda kutafuta maji unywe Panadol, kwa sababu mpaka sasa hivi natafakari jambo hili linasikitisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii ya kuchangia katika Wizara hii muhimu Bajeti ya Wizara ya Maji.

Kwanza kabisa nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo amekuwa akiitupia jicho Wizara hii ya Maji, kwa kuipatia bajeti kila mwaka wa bajeti na imekuwa ikiongezeka kwa kweli nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pili nikupongeze wewe Waziri, Naibu Waziri wako na timu nzima ya menejimenti katika Wizara hii ya Maji kazi yenu mnayofanya ni kubwa na mmeonyesha uwezo kama vijana mnatoa chachu kubwa na jinsi mnavyoisimamia hii wizara nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niwapongeze watendaji wenu ndani ya Mkoa wa Rukwa nikianza na meneja wa RUWASA Mkoa ndugu yangu Boaz na DM wangu Maganga pamoja na ndugu yangu Mkurugenzi wa SUWASA ndugu yangu Nzowa. Wanafanya kazi nzuri na tunawaamini sana mna vijana wazuri ndani ya Mkoa ya Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hii kabla sijaenda kwenye hoja nianze moja moja hapa kwenye jambo la watumishi, watumishi ndani ya hasa RUWASA. Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema kwenye Wizara yako hasa upande wa RUWASA ma–DM wengi na mahali pengine ma– RM wanakaimu zaidi ya miaka miwili, mitatu. Sasa brother kazi yako nikubwa na una wa–entrust watendaji hawa kwa mabilioni ya pesa kwenda kusimamia miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kuwakaimisha kwa muda mrefu hii ni jambo ambalo nakuomba waziri kaondoe hii dosari tunajua mmewafanyia probations ya kutosha zaidi ya miaka miwili, mitatu sasa kawa–confirm wawe proper wafanye kazi ya kusimamia Wizara yako na itaongeza ufanisi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; niliuliza swali ndani ya Bunge juu ya Miji midogo ya Laela na Mmpui hasa ukosefu wa maji hii miji inaisha tu kipindi cha masika baada ya hapo kunakuwa na shida kubwa ya maji. Hili jambo mmeji–commit kuanza kuchimba visima, lakini nikusisitizie kwa mji mdogo wa Laela solution narudia tena ni kutumia maji ya Mto Momba. Mmejipanga itahudumia karibia taarifa nzima ya Laela na ambayo hiyo mmejipanga kuanza upembuzi yakinifu.

Mheshimiwa Spika, naomba ulitupie jicho la pekee na ndugu yangu nakuamini nilikuletea wazo la kuchukua maji Kwela na sasa hivi ukaleta bilioni tano najua jambo la kumaliza tatizo la maji Mmpui na Laela liko ndani ya uwezo wako ndugu yangu Aweso ujawahi niangusha katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; niongelee jambo la wakandarasi. Umejitahidi sana na Wizara hii mnapata fedha nyingi, lakini kuna shida kubwa ya wakandarasi hasa wazawa. Kumekuwa na tendency moja ya wakandarasi kuwa na tamaa, wanaomba tender mikoa mbalimbali na wanakuwa na tender nyingi ikifika hatua execution wanashindwa ku– perform kwenye mikataba.

Mheshimiwa Spika, takupa mfano katika Jimbo langu la Kwela kuna mradi mmoja wa Ngomeni na kijiji kinaitwa Mpembano, mkandarasi alipewa kufanya zabuni yenye thamani ya shilingi milioni 940. Cha ajabu huyu bwana alikuja kuripoti site tukampa advanced payment ya milioni 100 badaye aka-abandon site akapotea.

Mheshimiwa Spiia, nawashukuru sana watendaji wako wa Mkoa wakiongozwa na Boaz walili–cover ile advanced payments bond ya shilingi milioni 100. Lakini tayari ilitakiwa atupe mradi ule Desemba, 2022 naambiwa mko kwenye process ya ku–terminate mmechukua muda mrefu wananchi wa Ngomeni na wa Mpembano Kata ya Lusaka wanasubiri kupata maji.

Mheshimiwa Spika, mkandarasi huyu ametuchelesha zaidi ya mwaka na ninaomba uende stepu mbili zaidi mbele msiishie tu ku–terminate contract lazima watufanyie watulipe liquidated damage hizi ambazo wamesababisha kwa kutuchelewesha.

Mheshimiwa Spika, pili, muwafanyie debarment mwende PPRA muwafungie. Hatutaki kuwa na wakandarasi ambao wanakuja kutuchezea wanaomba kazi kumbe hawana uwezo. Lakini pia nina miradi mingine inayoendelea kuna mradi unaitwa Mkunda Group pale ndani ya jimbo langu huo unapeleka maji Kata ya Kaengesa Kijiji cha Kaengesa A na B na kwenda Kianda. Mkandarasi huyu ilitakiwa amalize kazi yake mwezi Aprili, lakini mpaka sasa hivi ajajenga lile tenki na kuna kazi kubwa ya ku–supply mabomba.

Mheshimiwa Spika, ningeomba shughuli hii ya mabomba mfanye nyie wenyewe RUWASA kwa kutumia force account huyu hawezi kufanya hii kazi la sivyo utakuja kukuta huo mradi nao unaleta shida. Hali kadhalika mradi wa Iremba mkandarasi ni hivyo hivyo bilioni 1.9 tumempa hiyo kazi, lakini shughuli yake pale ameshindwa ilitakiwa naye akabidhi mwezi wa tatu hajakamilisha na inaoneka, chukueni basi ile part iliyobaki mfanye kwa force account.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika na mradi mwingine wa Lura Chitete huo ni mradi ambao pia ni muhimu sana ambao mkandarasi wake. Nina wakandarasi hao watatu niliokupa. Kwa mfano yule mkandarasi Kobeki wa Kwela anafanya kazi nzuri ni mtanzania mzalendo wakandarasi kama wale ndiyo tunawahitaji, umeampa kazi ndani ya muda mfupi amefikisha asilimia 75 na atatukadhi mradi mkubwa wa bilioni tano.

Mheshimiwa Spika, nikuombe Mheshimiwa Waziri katika jambo hili kaufatilie kwa umakini uwafanye review siyo wakandarasi tu ndani ya Jimbo la Kwela wakandarasi nchi nzima kawafanyieni performance appraisal muone je hawa tunawapa msiwarundikie kazi nyingi mtakuta mnawapa kazi nyingi wengine hawana uwezo wanafurahia tu ku–apply kazi mnawapa.

Mheshimiwa Spika, vilevile jambo lingine la muhimu ni juu ya vitendea kazi halmashauri yangu kwa maana ya Jimbo la Kwela tuna jiografia ambayo ni ngumu na inachangamoto ya miundombinu. Niombe sasa gari lile mlilotupatia limechoka brothe, fanya utaratibu mtafutieni DM ambaye anafanya kazi nzuri aweze kutekeleza majumu yake vizuri na hatimaye asimamie miradi ya mabilioni ya pesa mnayo peleka ndani ya Jimbo la Kwela.

Mheshimiwa Spika, pia niongelee suala lingine muhimu la Ziwa ya Tanganyika kwa maana ya hii project. Ulifanya commitment kubwa hapa jana na ukachukua na ku–quote maneno ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kwamba nia unayo na umejipanga na kujidhatiti, tunaomba sasa sisi tunatega sikio unapo wind up hotuba yako ya bajeti utuambie mpango kazi na mkakati ni upi juu ya kutoa maji Lake Tanganyika kwa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kweli tulikuwa na mijadala kwa Wabunge wa ukanda juu ya wewe kukushikia shilingi tunakusubiri kwenye ku wind up commitment gani unakuja nayo juu ya mradi huu wa kutoa maji Ziwa Tanganyika? Sisi hatuna shida tupe tu picha ambayo na ramani nzuri inayotekelezeka ili tujue mpango kazi aliyotupa Waziri ndani ya Bunge ni mpango kazi unaotekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, naomba nianze mchango wangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti hii mchango wangu utaanza kwa maswali kadhaa kama ifuatayovyo: -

Je, ni lini Serikali itaendelea au kusogeza huduma za kibingwa na kihadhi kimataifa/accreditation kwa hospitali kubwa na za kanda? Mfano wa Nyanda za Juu Kusini mojawapo ya hospitali inayosaidia karibu mikoa nane iliyopo ukanda huu ni Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (Mbeya Zonal Referral Hospital -MZRH).

Pili ni hospitali iliyo katika lango kubwa la nchi nyingi zilizo katika SADC kama lango kuu kwa upande wa Kusini; tatu, ipo katika mkoa ambao una barabara kuu ya kufikia nchi nyingine kupitia border za Tunduma na Kyela. Hivyo muingiliano wa wageni kutoka nchi jirani ni fursa kubwa ya kuzalisha utalii wa kimatibabu (Medical Tourism).

Mheshimiwa Spika, ikiwa patahitajika hospitali kubwa ya kuanza nayo kihuduma kwa wageni wa nchi jirani basi itakuwa ni hii MZRH. Hivyo ni fahari mno ikiwa hospitali hii itapewa kuwa kitovu cha utalii wa kimatibabu. Utalii wa kimatibabu utawezesha nchi za jirani au wageni kuja kupata huduma mbalimbali za kimatibabu na huduma bingwa kwa wepesi na ubora (fast & quality services).

Mheshimiwa Spika, umuhimu wa utalii wa kimatibabu ni kuwezesha kukua kwa pato la ndani la Taifa kupitia fedha za kigeni ambazo zitaingia nchini kwa wageni wanaokuja kupata matibabu na hata kujifunza baadhi ya huduma za matibabu za kibingwa kutoka kwa wataalamu wageni.

Mheshimiwa Spika, utalii wa matibabu na kujifunza teknolojia za matibabu kupitia hospitali hii kutaleta fursa ya muunganiko wa kujifunza hata wengine nao wanafanyaje na hata kuvutia uanzishwaji wa makambi (medical camps), nchi nyingine kwa ajili ya kutanua wigo wa huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, ipo haja kubwa kwa Serikali na wadau kuweza kuhakikisha hospitali zilizo katika lango la nchi jirani kuongezewa uwezo wa kupewa hadhi za kutoa huduma tambuzi kimataifa (international accredited) katika kufanya kazi na mashirika makubwa na taasisi kubwa za kimataifa.

Mheshimiwa Spika, kufanikiwa kwa hili kutasaidia sana kukuza hadhi za huduma, huduma za kibingwa kuvuka mipaka ya nchi na hata iwe zamu yetu sasa watu watoke nchi nyingine kuja kupata huduma kwetu kama ilivyo India ilivyojipa nafasi kimataifa kuwa na uwezo mkubwa wa kupokea wagonjwa na hata kutoa fursa za utalii matibabu.

Mheshimiwa Spika, kufanikiwa kwa MZRH kupata hadhi hii kutatanua wigo wa hospitali katika kuwa na uwezo mkubwa zaidi katika idara za maabara na ngazi zote za matibabu.

Mheshimiwa Spika, katika Nyanda za Juu Kusini basi mojawapo ya hospitali inayosaidia karibu mikoa nane iliyopo ukanda huu ni Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya.

Mheshimiwa Spika, ahsante na naomba kuwasilisha.
Hoja Kuhusu Bei ya Kuuza na Kununulia Mahindi
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza, naomba ni–admit jambo moja ambalo linaleta masikitiko. Wakulima wa mahindi wamekuwa wakipitia misukosuko mikubwa sana. Mwezi Mei na Juni huu ambao upo, mwanzoni bei ilikuwa imefika shilingi 80,000 shilingi 90,000 hadi shilingi 100,000. Ghafla tu ni kama Serikali hawakuwepo na hawakujua kama kutakuwa na jambo hili. Ghafla bei zilipokuwa hapo ndio wana–impose mambo mengi yanayojitokeza, documentation na nini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii imekuwa ni tendency kwa wakulima wa zao la mahindi yaani kila mwaka kuna jambo. Vile vile, kuna mtu mmoja anajaribu ku–admit kwamba ule mchakato ni rahisi na nini. Ungekuwa rahisi ungesababisha wanunuzi waje kirahisi. Hii inatokana kwa sababu hakuna competition. Mheshimiwa Waziri, jana amesema kwamba bei elekezi ni shilingi 800. Mahindi sio kama mafuta anayopanga bei elekezi. Bei ya mahindi inakuwa determined na competition kwa maana ya demand na supply. Kwa nini imeshuka? Ni kwa sababu supply ya mahindi ni kubwa na demand imepungua kwa sababu wanunuzi hawapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuache soko huru. NFRA najua watanunua lakini hata baadaye hawawezi wakanunua mahindi, najua sasa hivi hawanunui. Hata wakija hawana uwezo wa kununua mahindi yote. Turuhusu competition, wafanyabiashara wanunue. Hizi restriction tunakubaliana na jambo Serikali ililokuja nalo. Waahirishe mpaka mwakani ndiyo wajipange, lakini kwa mwaka huu tuache amani kwa wakulima wauze, nao wanataka wainue uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe tu, Mheshimiwa Bashe, aahirishe jambo hilo. Kwa sasa, hizo restrictions kama tutaendelea kwa namna tunavyoenda hivi, tunakwenda kumuumiza mkulima wa mahindi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na kukupongeza kwa kazi nzuri. Pia naomba kipekee nimpongeze Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa fursa hii nichangie kwenye hoja ya bajeti ya Wizara hii muhimu ya Ulinzi na Jeshi ya Kujenga Taifa na naomba niongelee unyang'anywaji wa mashamba Kijiji cha Luwa na Jeshi la Kujenga Taifa Kambi ya Luwa.

Mheshimiwa Spika, Jeshi limenyang'anya wananchi mashamba mnamo mwaka 2017 na mpaka kati ya jeshi na wananchi ni Mto Sopa lakini jeshi limevuka hadi kufika barabara ya mkoloni kuelekea Rukwa na kuchukua mashamba ya wananchi wa Kijiji cha Ntendo, Luwa na Fyengelezya.

Mheshimiwa Spika, kipindi mashamba yananyang'anywa, kuna mali ziliharibiwa sana kwani walipewa muda mfupi kuondoka eneo hilo. Kuna mifugo ilikufa (ng'ombe, mbuzi, kondoo, kuku na bata), pia kulikuwa na matanuli yaliyochukuliwa, nyumba tatu, mabanda ya mifugo, mazao ya kudumu ambayo ni matunda aina mbalimbali vipo shambani, majenereta na vifaa vya kilimo.

Mheshimiwa Spika, katika operation hii hakuna maongezi zaidi ya kuondolewa licha ya barua nyingi zilizoandikwa Serikalini bila majibu ya kuridhisha. Ushahidi ni nyumba zilizobaki pale maana hadi leo zipo.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri atoe majibu na afuatilie suala hii na kutupatia ufumbuzi wa mgogoro huu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa fursa hii, nami kuwa katika orodha ya wachangiaji kwenye bajeti hii muhimu ambayo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa letu.

Mheshimwia Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya hasa katika sekta hii ya uchukuzi. Ameijali, na amekuwa akiijali kila wakati na kuipa bajeti ya kutosha kuendesha mambo yao wakati kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Profesa Mbarawa na wasaidizi wake Manaibu, kazi yao ni nzuri na tunawapongeza sana. Vile vile watendaji walio chini yake, Katibu Mkuu na Watendaji wa Taasisi zilizo chini yao, nikianza na TPA pale, na bahati nzuri tuna kijana mzuri pale MD wa TPA Mbossa, na ndugu yangu Mativila wa TANROADS na wengine wote wanafanya kazi nzuri, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mchango wangu leo nitakuwa na mambo mawili muhimu. La kwanza, nitaongelea mambo ya Mkoa wangu wa Rukwa, na pili nitakuja kushauri mambo makubwa kwa mustakabali wa Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri, juzi alikuja mkoani kwetu kwa ajili ya kuanza mkataba wa kuanza ujenzi wa ndege pale Sumbawanga, halikadhalika Barabara yangu ile ya kutoka Mutendo – Muze ya zaidi ya Shilingi bilioni 45 pamoja na Barabara ya Mathai kwenda Kasesha, tukupongeze, na kweli tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutujali kwa kiwango kikubwa Mkoa wa Rukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hayo, kuna jambo ambalo ameliongea hapa kwa msisitizo mkubwa kwenye hotuba yake, nilikuwa namsikia kwa umakini Profesa, juu ya meli kwenye Ziwa Tanganyika. Sisi uchumi wa mikoa mitatu hiyo kwa pamoja kwa maana ya Rukwa, Katavi na Kigoma tunategemea sana hiyo meli lili ika-boost uchumi wa maeneo hayo matatu. Ni sehemu ambayo nchi tunazopakana nazo kwa maana ya Burundi, DRC na maeneo mengine kama Zambia, yana bidhaa nyingi wanazozitegemea kutoa mikoa hiyo mitatu niliyoitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu sana. Mwaka jana tulimpigia kelele hapa Bungeni juu ya meli, akatuahidi. Hivi leo amesema mwezi ujao Juni, mkandarasi ataanza kazi. Bahati nzuri, commitment aliyoifanya hapa iko kwenye interval ambayo tutakuwa humu Bungeni, na tutakuwa hatujachangia Bajeti Kuu ya Serikali. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, wananchi wana matumini makubwa na ahadi aliyotoa leo. Unaona katika maeneo mengine wana meli tano, sita, saba, lakini Ziwa Tanganyika lime-collapse, na ni ziwa ambalo linatu-link na nchi ambayo tukiwekeza vizuri, mikoa hii ita-boost na tutaongeza pato la Taifa. Kwa hiyo, naomba jambo la meli, tuko serious tumekaa nawe katika vikao vingi, naamini baada ya bajeti tena tutakaa utupe mpangokazi ili sisi wawakilishi wa maeneo hayo, tuwe na Imani sasa kwamba mnaenda ku-address tatizo la Lake Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namwomba Profesa, Barabara ya Ntendo – Muze ile alienda kufanyia endorsement kwa maana ya kwenda kumkabidhi mkandarasi, kazi inaendelea vizuri, lakini kwa bonde langu la Ziwa Rukwa ambapo Barabara yote hii kwa urefu ni kilometa 200, Ntendo – Muze mpaka Kilyamatundu ni Kilometa 200. Kule ndani ya bonde la Ziwa Rukwa sasa hivi kuna shughuli kubwa inaendelea ya exploration, ambayo tuna wawekezaji wa gesi ya Helium, ambao wame-invest zaidi ya kufanya tu utafiti zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii Barabara ina umuhimu mkubwa kwa sababu uchimbaji unaanza wa majaribio mwezi wa Nane. Kwa projections zilizopo, helium iliyopo bonde la Ziwa Rukwa inaenda kutupatia pato la Taifa zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 100, ndani ya miaka mitano tutakuwa tuna-hit Dola za Kimarekani milioni 500. Kwa hiyo, hata hii investment tutakayoiweka kwenye Barabara hii itarudi ndani ya muda mfumi kwa sababu uchimbaji wa gesi ya Helium itakayofanyika pale itakuwa na impact kubwa, siyo tu kwa Mkoa wa Rukwa, lakini itakuwa na mchango mkubwa kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba hii Barabara tuiongezee sasa bajeti. Ina umuhimu, sio kwa Mkoa wa Rukwa lakini uchumi mkubwa wa Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Profesa, hili jambo akalimalize, kipande kile akiongezee hela, kilometa 200 zote ziwe kwenye operation zikamilike kutoka Muze mpaka Kilyamatundu pale na baadaye kwenda Kasansa kwa ndugu yangu pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongelea mambo ya jimboni, nije kwenye mambo muhimu ya kitaifa, na hapa profesa naomba tusikilizane kwa umakini. Kuna mambo mawili ambayo yamekuwa yaneleta dosari kubwa sana kwenye Wizara hii na dosari hii imekuwa ya muda mrefu na kila mwaka unavyoendelea dosari hii inazidi kuwa kubwa. Mambo mawili, riba kwa wakandarasi. Riba kwa wakandarasi imekuwa ni jambo ambalo linaumiza taifa hili. Mwaka 2021/2022 wa fedha uliokwisha, tutachulia tu shirika moja kama TRC, tulilipa riba ya Dola za Kimarekani 1.34 kwa sababu tu tumeshindwa kulipa certificate 24, na Profesa haya mambo yako ndani ya uwezo wako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna jamnbo la VAT exemption, ucheleweshaji, na haya yanafanyika kwenye Wizara ya Fedha ya ndugu yangu Mwigulu Nchemba, yanaletwa pale exemption zinachelewa. Mwaka jana. na nachukulia mfano wa TRC, tulilipa bilioni 8.35, kwa ajili ya kwamba exemption (riba) imechelewa. Sasa Profesa, leo hii nataka kesho utakapokuwa una wind-up bajeti yako utueleze umejipangaje kuondoa tatizo la kulipa penalty na hizo riba zisizokuwa na msingi? La sivyo, mimi binafsi nitataka shilingi yako utueleze umejipangaje. Bado tunakusubiri Novemba, baada ya kuja kujadili hapa ripoti ya CAG. Hizi taasisi zako zinapewa bilioni nyingi za fedha na riba inapotokea ni billions of money, ukizisoma zimekuwa zinakuwa kila mwaka. Sasa hii inatupelekea sisi ambao tunakuja ndani ya Bunge hili na pengine wewe mwenyewe tatizo hili halikuumi; ninaamini sasa kwa sauti yangu leo humu Bungeni utakwenda ku- take action, mfute riba, kwa sababu miradi mingine riba haina maana. Tunakuwa tumepewa fedha za mikopo na World Bank au taasisi nyingine, fedha iko pale, sasa mnapataje riba ilhali hela zipo, kazi imefanyika mme-certify, mnashindwaje kulipa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia VAT exemption haiwezi kuwa tatizo kwenye nchi, ni internal communication ndani ya Serikali, Wizara yako na Wizara ya Fedha; na bahati nzuri fedha hizi zinatoka Wizara ya Fedha zinakuja kwako kwenda kwenye utekelezaji lakini VAT ambayo iko ndani ya uwezo wetu inatusababishia tulipe riba ya bilioni nane na bilioni nyingi za fedha. Kwa kweli profesa hili hatutakuelewa, tunaomba mje mtuambie mmejipangaje kwenye Serikali ili kukomesha tatizo la riba kwa wakandarasi ambalo linagharimu taifa na VAT exemption hizi ambazo ziko chini ya uwezo wetu kama Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niongelee suala lingine, variation kwenye Miradi. Miradi hii inakuwa designed, maana tunafanya upembuzi yakinifu, tunakwenda kwenye detailed designed, tunakwenda kutanga za tenda, ghafla unakuta kuna variation zinakwenda asilimia 20, 30, 40, na baadaye unasema au kulikuwa na mchezo wa ku-skip baadhi ya item ili tuje tutumie room ya variation kufanya mambo yetu? Profesa hili jambo ukapitie kwenye taasisi zako kwenye miradi mikubwa kama vile TRC, TANROAD, ATCL na taasisi zote, huko una mabilioni ya fedha. Suala la variation limekuwa ni ugonjwa mkubwa ambao hauleti afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nafikiri muda umekwisha nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa kwa kuchangia kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kwa moyo wangu wa dhati kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya hasa katika kuwezesha uhuru wa vyombo vya habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii Mheshimiwa Nape na Naibu wake Mheshimiwa Kundo kwa jitahada kubwa zinazofanywa na katika Wizara hii na Serikali ya kuboresha sekta ya habari na mawasiliano nchini bado mkoani Rukwa hususani Jimbo langu la Kwela kuna changamoto bado zinatukabili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumfahamisha Mheshimiwa Waziri kuwa Mkoa wa Rukwa ni takribani miaka mitatu sasa hatuna reporter wa television ya Taifa (TBC) toka aliyekuwa reporter Mzee Nswima Ernest kustaafu. Mheshimiwa Waziri ifahamike kuwa TBC ni kituo kikubwa cha habari katika Taifa letu, hivyo kutosikika kwa takribani miaka mkoani kwetu tunapoteza fursa nyingi zikiwemo za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Waziri kuwa katika Jimbo langu kuna maeneo ambayo mawimbi ya TBC FM hayakamati kabisa katika Kata za Milepa, Lusaka na kadhalika, wanapata habari za TBC kupitia runinga kwa wale wenye ving'amuzi ambao ni kundi dogo sana hasa wale waliokaribu na miji changamfu. Mkoa wa Rukwa una vivutio vingi vya kiutalii kama Kalambo falls, fukwe za Ziwa Tanganyika, game reserve na Ziwa Rukwa, lipo Ziwa Kwela na vivutio vingi vya asili vitokanavyo na desturi na tamaduni za Wanarukwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa TBC FM kwa baadhi ya maeneo, tumepunguza wigo wa kutangaza utajiri wa mkoa wetu kwa ukosefu wa TBC reporter na kutokuwepo kwa mawimbi ya TBC FM katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni baadhi ya vyombo vya habari vilivyo nje ya Mkoa wa Rukwa kutoa habari zisizo na uhalisia, zenye maudhui ya kutisha wageni na hata wawekezaji juu ya Mkoa wa Rukwa na kusababishia mkoa hasara za kiuchumi. Kwa mfano vyombo vingi vya habari vimekuwa vikitoa maudhui mbalimbali kwa kutumia jina la Sumbawanga vikihusisha matendo ya kishirikina na uchawi jambo ambalo si sahihi na halipaswi kufumbiwa macho na taasisi kama TCRA na nyingine zenye mamlaka husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumuomba Mheshimiwa Waziri apokee changamoto na tatizo kubwa la huduma za mitandao yaani kukosekana kwa minara ya simu inayofanya kazi kwa saa 24 kwa baadhi ya maeneo ya Jimbo la Kwela lililopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, Mkoa wa Rukwa. Kwa mfano kuna tatizo sugu hasa Kata ya Milepa kwa Vijiji vya Milepa, Kinambo, Msia, Kisa na Talanda. Mnara uliopo Kijiji cha Milepa ambacho ndipo yalipo Makao Makuu ya Kata haufanyi kazi saa zote kwani unafanya kazi kwa saa tano tu yaani unawaka kuanzia saa 3:30 asubuhi hadi saa 9:00 alasiri unakuwa umezima na siku kukiwa na mvua au mawingu basi mnara huo hauwezi kuwaka kwa siku nzima tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kijiji hiki kinazo taasisi zinazohudumia wananchi kikiwemo Kituo cha Afya Milepa, Kituo cha Polisi, kituo cha kukusanyia mapato ya Halmashauri kilicho na Pashine ya kukusanyia mapato (POS machine), sekondari ya kata, shule za msingi zipatazo sita na ofisi za utawala ngazi ya kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma hizi zote zimefungiwa mifumo ya malipo na ya mawasiliano kupitia mitandao, hivyo kuanzia saa 9:00 alasiri hadi kesho yake saa 3:00 asubuhi hakuna huduma inayofanya kazi kupitia mtandao na hivyo husababishwa huduma zote za umma kuzuiwa kufanya kazi kupitia mitandao ikiwa ni pamoja na kutoa risiti zote kupitia mifumo kuanzia huduma za malipo ya ushuru. Usajili wa wagonjwa kimfumo, kutoa risiti kwa wagonjwa wanapokuwa wanataka kulipia gharama za matibabu, kutoa taarifa mbalimbali za kiuhalifu polisi, kutoa taarifa zozote kwenye Idara za Elimu na Utawala yaani huduma hizi zote husitishwa kutokana na mnara kuzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi zimetokea kesi mbalimbali na kupelekea vifo hasa kwa akina mama wajawazito baada ya kukosekana mawasiliano pindi wanapohitaji huduma ya gari la wagonjwa lililopo Kituo cha Afya Milepa ili likawachukue wajawazito walioshindwa kujifungua kwenye zahanati zilizopo nje ya kituo hicho, lakini huduma hiyo hukosekana kutokana na kutokuwepo kwa mawasiliano kunakotokana na kuzima kwa mnara wa Vodacom ambao ndiyo mnara pekee uliopo kijiji hiki cha Milepa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hiki cha afya kinahudumia kata zipatazo saba zenye zaidi ya wakazi 108,700 lakini eneo wanalolitegemea kupata huduma muhimu ndilo hili ambalo tatizo la mtandao ni shida kubwa sana. Kutoka Kata ya Milepa kilipo Kituo cha Afya hadi kata ya mwisho ambayo ni Kilangawana ni zaidi ya umbali wa kilometa 125 hivyo utaona ni namna gani mgonjwa hasa mama mjamzito endapo mawasiliano yatakuwa hayapo atakavyoshindwa kuokolewa mapema pindi uhitaji wa gari utakapokuwa unahitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo madaktari wanapofanya huduma kubwa hasa za upasuaji huhitaji wakati mwingine kuwasiliana na madaktari bingwa hasa linapotokea tatizo kubwa lakini hushindwa kufanya hivyo kutokana na aidha muda huo kunakuwa hakuna mawasiliano. Pamoja na tatizo hili kuwepo, umeme wa REA upo na umepita umbali wa mita 400 kutoka mnara ulipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengine yenye changamoto za kukosekana kwa mawasiliano kwa njia ya simu ni pamoja na vijiji vya Kizumbi, Kamnyaza na Mpembano Kata ya Lusaka, vijiji vya Katoto na Kazi Kata ya Lyangalile; vijiji vya Zimba, Misheni Kata ya Zimba; vijiji vya Mtetezi na Kapewa Kata ya Mpui na vijiji vya Msila na Kasekela Kata ya Mfinga vyote vipo ndani ya Jimbo la Kwela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba msaada wa haraka ili kuwasaidia wananchi hawa katika sekta ya mawasiliano kimtandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naomba kuunga mkono hoja.