Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Jesca Jonathani Msambatavangu (1 total)

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumekuwa na matatizo na vijana wetu wanaotoa huduma za usafiri mijini ikiwemo bajaji, bodaboda na daladala na hasa kutokana na kugombania ile miundombinu ya barabara. Nilichokiona sasa pale, pamoja hiyo crisis iliyopo ni kwamba kuna shida katika ku-co-ordinate namna ya kufanya kazi zetu kati ya Serikali za Mitaa na Wizara. Mzigo mkubwa…

SPIKA: Ukichukua muda mrefu, hutajikuta umeuliza swali.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Swali lenyewe lilivyo, kidogo linahitaji ufahamu. Samahani.

Mheshimiwa Spika, jinsi ilivyo sasa tunapata shida kwa sababu unakuta kwa mfano TARURA wapo TAMISEMI wakati Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ndiyo inayohusika na masuala ya ujenzi na miundombinu. Sasa unapofika wakati wa kufanya co-ordination, hawa Ujenzi wanakuwa kwa mfano wamejenga barabara kubwa imepita katikati ya mji, lakini TARURA hawakuwa aware kutengeneza alternative way kuhakikisha kwamba ule mzigo mzito wa traffic unaokuja kuingia kwenye ule mji unapitishwa kwenye barabara nyingine. Labda ni kwa sababu TARURA wapo chini ya Wizara nyingine. Haya yanatukuta pia kwenye masuala ya afya…

SPIKA: Swali lako ni nini sasa? Maana unachangia.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Haya yanatukuta pia kwenye Wizara ya Afya kwenye kupandisha hospitali zetu kutoka vituo kwenda Hospitali za Wilaya.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu ni hivi: Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kuona kwamba hizi Wizara zinachukua mzigo wake mzima; kwa mfano, Ujenzi na Uchukuzi wanaichukua na TARURA, Wizara ya Afya wanachukua na vituo vyake vya zahanati ili wanapotaka kupandisha madaraja washughulike wenyewe, kusiwe na contradiction na kuleta ugumu pale katika kurahisisha kazi hiyo? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Msambatavangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake limegusa mambo mengi; limegusa bodaboda, TARURA, TANROAD baadaye akahama tena akaja kwenye hospitali. Kwa hiyo, halina mwelekeo sahihi sana, lakini nataka niseme tu, ndani ya Serikali vyombo vyote ni vya Serikali na tumetoa miongozo ya kila mmoja. Miongozo hii tumejitahidi lazima izungumze pamoja. Ninaposema lazima miongozo izungumze, maana yake mipango ya TANROADS hata kama inaenda kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, lazima pia kama ni ya kisheria iende i-fit in; iweze kuwa ndani ya mipango ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, wanapojenga barabara kukatiza humo, ni lazima barabara hiyo ijengwe kwa vipimo vilevile na Mamlaka ya Serikali za Mitaa ziruhusu hawa wapitishe barabara hiyo ili iweze kutumika na wote. Hata kwenye matumizi, kila mmoja atatumia na kama barabara hiyo inahitaji kuwa na njia za waenda kwa miguu, lazima ziende hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa tunapokuja kwenye Sekta ya Afya na yenyewe ambayo inaongozwa na Wizara ya Afya ambapo pia miundombinu inajengwa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, ni lazima Wizara hizi zizungumze, zihakikishe kwamba zinasimamia ujenzi wa miundombinu hiyo ili iweze kutoa huduma kwa Watanzania. Mwisho wa yote haya tunawahudumia hawa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, sasa tunapokuja hapa ndani ya Serikali, tunaweka sawia katika mambo ya kisheria ambapo kila mmoja atatumia miundombinu yote ya kila Wizara kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni zilizopo na zinazotuongoza. Kwa hiyo, niseme tu kwamba taasisi zote hizi pamoja na kwamba zipo huko kwenye mamlaka mbalimbali, lakini lazima ziwe zinazungumza lugha moja ili Mtanzania anapotumia asiwe na mgongano wa matumizi ya maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama nilivyosema swali lako lilijikita kwenye mambo mengi, lilikuwa pana, nilichofanya ni kuchukua maeneo hayo yote na kazi wanazozifanya kuwa zote ni za Serikali na kila mmoja anapotaka kutekeleza lazima kuwe na mawasiliano na taasisi nyingine ambayo ni ya Serikali. Kwa hiyo, Serikali lazima izungumze lugha moja na utoaji huduma lazima uende wa aina moja ili wananchi waweze kupata huduma kwenye maeneo hayo, kila mmoja na eneo ambalo analolihitaji. (Makofi)