Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jesca Jonathani Msambatavangu (28 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi na nawashukuru wote kila mmoja kwa nafasi yake aliyechangia uwepo wangu mahali hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kupokea Hotuba ya Rais kwa mikono miwili na nampongeza sana kwa sababu sisi kama Wabunge, tumepokea dira na tumepata kitendea kazi cha kufanyia kazi katika uwakilishi wa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naanza na sekta ya utalii, katika ukurasa wa 46, Mheshimiwa Rais ameongea kwamba ni sekta ambayo itawekewa mkazo mkubwa kutokana na umuhimu wake katika Taifa letu; kwanza, katika mchango wake mkubwa katika kuongeza pato la Taifa, pia ni sekta ambayo itatoa ajira kwa vijana wetu kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza upande wa Serikali; wenzetu hili wameshalianza, nasi watu wa Kanda ya Kusini au Southern Socket Tourism tunawashukuru sana kwa sababu tumeletewa mradi mkubwa wa REGROW ambao umetengewa dola milioni 150 kwa ajili ya kuendeleza utalii kusini; Iringa pia haikuachwa, itakuwa hub ya utalii huo, nasi tumepewa dola milioni sita kwa ajili ya kuanzisha Tourist Resource Center pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru sana kuhusu msitu wa Kihesa Kilolo. Namshukuru Waziri wa Maliasili, tumeongea hili na amelifanyia kazi kwa haraka sana. Naamini ujenzi unaanza pale mara moja ili nasi southern socket au ukanda wa kusini tuwe sehemu ya kuchangia pato la Taifa kupitia utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba, ili utalii uweze kuwa mzuri, tunahitaji kuboresha huduma zetu kwa watalii. Kwanza, naomba tuboreshe huduma ya upatikanaji wa ubadilishanaji wa fedha za kigeni. Watalii wetu wengi wanapokuja kwenye zones za utalii wanakosa huduma hii kutokana na mchakato ambao ulipitishwa kwenye maduka yetu ya kubadilisha fedha za kigeni. Kwa hiyo, tunaomba Serikali iangalie hasa kwenye hizi nyanda za utalii, ni namna gani inalegeza masharti ili tuweze kuwahudumia watalii na lile neno lao, watakaporudi tutapata watalii zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuhusu kuboresha huduma za miundombinu, tunaomba barabara. Tumeshaanza kuboreshewa kiwanja cha ndege, sasa tunaomba barabara ile ya National Park, watakaposhuka pale ile barabara ya kutoka Iringa mpaka Ruaha National Park ya kilometa 104 basi nayo iboreshwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwenye suala la elimu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ukarabati mkubwa uliofanyika kwenye Shule za Sekondari kongwe, tunaomba juhudi zile zile zielekezwe kwenye shule zetu za msingi kwani nazo zimechakaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mtaala haliepukiki, tunaomba Wizara ya Elimu tujipange kubadilisha mtaala kwa watoto wetu ili watoto wetu waweze kuajirika na kujiajiri nje na ndani ya nchi yetu. Tunaomba sana elimu ya kujitegemea irudishwe kwenye shule zetu ili watoto hawa wanapotoka waweze kujifunza kujitegemea. Vile vile tunaomba kuwe na masomo compulsory kama ya ujasiriamali kuanzia kwenye level ya shule ya msingi ili watoto waweze ku-develop visions zao wenyewe tangu wakiwa wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru sana kwamba kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais pia amesema kutakuwa na program mbalimbali za mafunzo ya ujuzi na maarifa ili kukuza uchumi. Tunaomba sasa vyuo vikuu vilivyoko kwenye zones zetu na mikoa yetu, kama kile Chuo Kikuu cha Mkwawa, kiwe independent, kiweze kusimama chenyewe ili kisaidie kutengeneza program zao kwenye kanda zetu zile ili kuwasaidia watoto wetu waweze kupata maarifa ya kufaidika na mazingira yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tusiendelee kuwa ni Vyuo Vikuu Shirikishi halafu vinaendelea kupokea program zinazopangwa Dar es Salaam wakati kule kule zinge-scan mazingira ya kule, zingepanga program za kule kule, zitawasaidia wananchi wetu. Tunaomba sana hili lichikuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la uchumi, tunashukuru kwa ajili ya uzalishaji, lakini tunaomba sana mafunzo ya ujasiriamali yatiliwe mkazo kwa sekta binafsi lakini kwa informal sector na formal sector. Tunaomba makundi yale ya Madereva, Wamachinga, makundi ya bodaboda, yapewe mafunzo ya ujasiriamali ya kimkakati kutokana na kazi zao. Mafunzo ya ujasiriamali yasiandaliwe tu kwa ujumla, lakini yaende specific. Kwamba hawa ni Mama Ntilie, katika sekta yao tunawaboresha vipi? Hawa ni madereva wa bajaji, katika sekta yao tunawaboresha vipi? Tusitafute kupeleka mafunzo ambayo ni mafunzo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika moja. Kulinda tunu za Taifa, naomba hili niliseme. Hapa yameongelewa masuala…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jesca kuna majina mengi hapa mbele. Ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Mimi nitaongelea jambo moja tu kuhusiana na urasimu katika utekelezaji wa Mpango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaomba nitoe mfano mmoja ambao uliwahi kutokea hapa kwetu, inaweza kuwa siyo hadithi nzuri sana, lakini itatusaidia kukumbuka. Kuna wakati fulani ilitokea hadithi ya mafuta ya upako; yalimwagwa kwenye carpet na watu wakapita wakiwa na malengo ya kupona pale, huzuni zitabaki pale, wakiwa na malengo kwamba kama waliingia na mawazo, yataisha pale na kwamba wataondoka hawana stress. Sasa basi, Mpango huu naufananisha kama mafuta ya upako, kumbe ndani ya yale mafuta ya upako kulikuwa kuna utelezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya watu kutoka wamepona pale, wakawa wanakatana mitama mle, wanalaliana, wanakanyagana, wengine wakatoka wamekufa, tukapata majeruhi na wengine ambao walikuwa mahututi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango ni mzuri na mambo yamekaa vizuri. Wasiwasi mkubwa ni urasimu ambao hauna maana katika utekelezaji wa Mpango. Lazima tukubaliane sasa kama tunakwenda kama nchi, tushirikiane mihimili yetu yote mitatu, Wizara zetu zote, pamoja na Idara zetu zote, tushirikiane na vyombo. Kwa sababu kuna wakati fulani tunaweka mipango mizuri lakini unaweza kukuta kuna mahali tunaweka vitu ambavyo vinasababisha tusiende mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tumeongea kwenye Mpango kwamba tuna miradi ya kimkakati. Miradi hii mingine imeanza siku nyingi, bado inahitaji gharama ndogo sana. Sasa kwa sababu ya urasimu usiokuwa na maana, utakuta kuna vikwazo vinatokea tu ama kutoka katika Idara moja ama kutoka katika Idara nyingine au kutoka katika Wizara fulani au kutoka katika chombo fulani tunakuwa hatuendi mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tuna miradi kwa mfano ya utalii, tayari tuna capital kule kwa sababu tayari tuna Wanyama, tuna Mbuga za Wanyama, tuna kila kitu. Kuna miundombinu tu kuielekeza kufika kule kwenye utalii ili sisi tuanze kukamua dola, kunaanza kutokea urasimu usiokuwa na maana. Halafu wakati mwingine ku-connect sasa; tumeboresha viwanja vya ndege, tumenunua ndege, zinafika kwenye viwanja vya ndege. Kutoka pale kwenye kiwanja cha ndege kufika kwenye Mbuga ya Wanyama hapaingiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huu ndiyo tunasema utelezi kwenye upako. Utelezi ndani ya Mpango, kwa nini sasa? Hii miradi ya kimkakati kama ya utalii ambayo inaweza ikatengenezewa tu miundombinu na tukaanza kupata fedha, isitolewe hiyo fedha tukafanya mambo haya na tukatekeleza ili tuanze kukamua hela huku wakati huo huo tukiboresha huduma zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tuna Wizara ya Viwanda na Biashara, tuna Wizara ya Vijana na Ajira, wanafanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba wanatengeneza ajira kwa vijana wetu. Tuna Wizara zinafanya juhudi kubwa au Idara zinafanya juhudi kubwa kuua vyanzo hivyo vya ajira. Ndiyo maana hapa unakuta Waheshimiwa Wabunge tunakuja kulalamika, ni kwa nini bodaboda zijae kwenye Vituo vya Polisi na vijana wetu wakati wamejiajiri na tumeruhusu kama sehemu ya ajira? Huo ndiyo unakuwa utelezi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tumekubaliana kwamba tunavutia wawekezaji kwenye Taifa hili. Tuna Wizara ya Uwekezaji kwenye nchi yetu, tulikuwa na TIC wakati ule inavutia wawekezaji kwa kuweka mazingira mazuri. Kuna Idara nyingine wanapofika ndani ya hii nchi, wanazuiliwa vibali, wanaanza kuwekewa urasimu wa vibali kibao, sijui kodi, vitu kama hivyo. Huo ndiyo utelezi sasa kwenye Mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka uchumi shindanishi kikanda na Kimataifa. Leo hii tunataka Watanzania wakauze bidhaa kwenye Soko la Afrika Mashariki, Soko la SADC na Soko la AGOA. Rudi sasa kwenye utelezi; namna ya kupata Passport, namna ya kupata Hati tu ya Uraia, namna ya kupata cheti cha TBS, utelezi! Kina Mama wanatengeneza products zao, kuwekewa tu alama ya TBS kuna milolongo mirefu, akina mama wanashindwa kwenda mbele, tunashindwa kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine tunadanganyana humu. Unapofuatilia kibali kwa ajili ya wawekezaji au kuleta wawekezaji, utasikia kuna vyombo, kuna vyombo, kuna vyombo; sasa sijui ni bakuli, sijui ni thermos, sijui ni chupa! Vinazuia! Hapa vyombo vinafanya utafiti, uongo mtupu! Tunadanganyana, tunaweka utelezi kwenye Mpango. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tuna miradi mikubwa ya umeme hapa imeanzishwa, kama Julius Nyerere Stiegler’s Gorge. Ule ni mradi ambao utatusaidia. Wapo Watanzania wanaubeza, zipo Idara nyingine ni utelezi. Wapo Watanzania wengine hawaoni umuhimu. Mradi ule utatuongezea nguvu ya umeme, utatupunguzia production costs, utasababisha bidhaa zetu kushuka bei. Hivyo utasababisha nasi tuweze ku- compete kwenye soko la East Africa na Kikanda. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi ule ukiwekwa maji pale, umeshatengewa tena hekta zaidi ya 150,000 kwa ajili ya irrigation scheme unakwenda kwenye ile irrigation, utakutana na watu wa bonde. Utelezi hutuzuia sasa tushindwe kufanya irrigation schemes. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuna vitu ambavyo nasema kama hatutashughulika na utelezi kwenye mafuta ya upako, tutaondoka tumekufa, tutaondoka majeruhi. Lazima Serikali yenyewe ijipange. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nilikuwa nasoma taarifa ya CAG, anaongelea kuhusu kukusanya mapato na TRA jinsi ilivyokusanya, lakini moja ya mapendekezo ya CAG, aliwapa mapendekezo kama 338; ni asilimia 19 tu wameyafanyia kazi, mapendekezo 266 wameshindwa kuyafanyia kazi. Asilimia 38 ya mapendekezo 266 ni kwa sababu yako Idara nyingine, kwa hiyo, yameshindwa kutatuliwa, Idara nyingine imeleta utelezi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ndugu zangu kama hatutaangalia haya na kuangalia urasimu tuliouweka ambao unatukata mtama wenyewe kwenye upako, hatuwezi kufika mbali. Lazima sasa Serikali iamue kwa nia ya dhati kuondoa urasimu usiokuwa na maana. Kama tumeamua tunajenga ajira kwa vijana wetu, walindwe; machinga walindwe; bodaboda walindwe; na mama ntilie walindwe. Wale hawajaenda shule lakini tuna wasomi, Maafisa Biashara wetu, siyo kazi yao kuingia kuwasumbua wale, ni kwenda kuwaelimisha wafuate taratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kazi ya Jeshi la Polisi tu kukamata bodaboda peke yake, ni kutoa na elimu. TRA leo ni chombo kinachokusanya mapato, siyo kazi yao kuwa innovator wa kesi kwenye nchi hii. Zipo kesi za biashara kwenye Mahakama ya Rufani 1,097 ambazo ziko created na TRA, wamehama kwenye lengo lao la msingi, wamehamia kwenye ku-create kesi. TRA wana kitengo cha kutoa elimu kwa wafanyabiashara, watoe elimu kwa wafanyabiashara na sio kuwavizia wafanyabiashara wamekosea ili wao wapate mazingira ya kuwashtaki. Kwa hiyo lazima tuondoe utelezi na urasimu usiokuwa na maana, twende tukatekeleze hii miradi ya kimkakati. Tujenge barabara kwenda kwenye National Parks zetu. Kwa mfano sisi tuna barabara ya kutoka Iringa - Ruaha National Park, ni park ambayo ni ya pili kwa ukubwa duniani. Ina tembo wakubwa kuliko National Park yoyote lakini miaka yote barabara iko kwenye Ilani lakini haitekelezeki mahali ambako tungekwenda kuchukua dollar bure. Unaona watu wanaingia Serengeti wanakwama kule ndani, wakati vitu tayari viko pale. Tuache, twende tukaamue sasa kufanya kazi kwa ajili ya ku-implement Mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo tutakwenda vizuri. Tukiangalia hawa watu wa chini, ameongea Mheshimiwa Mbunge mmoja kama tukiangalia hii micro enterprise ya wafanyabiashara wadogo tukaielimisha, leo tunaongelea ujuzi, kutoa elimu ya ujasiriamali. Tuna mkakati gani wa kuwapa hiyo elimu? Tunawapa mafunzo ya ujasiriamali kwa mtindo gani? Au tumeweka tu tunatengeneza mifuko ya wajasiriamali, sijui ya wafanyabiashara wadogo wadogo, hiyo mifuko inaishia juu. Kuna mmoja amesema hapa kuna Benki ya Kilimo ina majengo mazuri Dar es Salaam, Dar es Salaam kuna kilimo gani? Haya ndiyo mambo ya utelezi, yaani vitu ambavyo watu wanatengeneza dili ambazo hazieleweki! Twende kwenye grassroot tukatatue matatizo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaongelea akinamama wajengewe vituo vya afya, zahanati na hospitali, huduma za uzazi ziwe bure, wewe unakaa unazuia fedha ya matibabu kwa akinamama wasitibiwe, una hila gani? Utelezi huu. Sisi tunataka kuongeza wapigakura kwenye nchi hii, tunataka kuongeza raia bora kwenye nchi hii, wazaliwe watoto bora kwenye nchi hii, unazuia fedha bila sababu, huo ni utelezi. Tunataka sasa urasimu na Wizara zijione kama kila Wizara ina heshima, maana ipo ile kuona kwamba labda Wizara hii kwa sababu sisi ni Fedha, basi ni wa muhimu sana, samahani kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu, wewe ni rafiki yangu sana. Labda wewe ndiyo wa maana zaidi kuliko yule Waziri wa Wizara ya Kilimo au Waziri yeyote, hapana! Kwa sababu ili Waziri wa Fedha awe na fedha, ni lazima kilimo kichangie mapato, ili awe na fedha, lazima bodaboda wachangie, ili awe na fedha, lazima mama ntilie wachangie. Leo hii tuna vitu vya ajabu, tunatakiwa kuangalia mambo ya utelezi, urasimu wa kijinga. Kwa nini tusifikirie Watanzania wetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imegonga Mheshimiwa…

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: … wanaofanya vizuri tukawatumia sisi wanaanza kuonekana kutumika kwanza Afrika Kusini.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja lakini utelezi uondolewe. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami nitumie nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niongelee tu kwa ujumla sekta hii ya usafirishaji, kwanza sifa zake mahususi kiulimwengu ili sekta hii ionekane iwe bora. Sifa ya kwanza, ni lazima kuwe na mifumo mizuri iliyotengenezwa ya usafirishaji kwenye miji au tunasema well designed inter-city systems. Sifa nyingine ni ku-avoid unnecessary traffic flows au tunasema ni kuepuka ile misongamano isiyokuwa ya muhimu.


Mheshimiwa Naibu Spika, sifa nyingine ni kuhakikisha kwamba mifumo ya usafirishaji inapunguza gharama. Sifa nyingine ni kuhakikisha mifumo ya usafirishaji wetu inakuwa salama na ya uhakika. Nyingine ni kuhakikisha kwamba tunaweka mifumo mizuri ya usimamizi ya miundombinu yetu ya usafirishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichangie pale kwenye kuweka mifumo mizuri ya usafirishaji kwenye miji yetu. Ndugu zetu hawa wa Wizara ya Ujenzi wao ni wataalam na bahati nzuri sana Waziri tuliyenaye alikuwa Katibu wa Wizara hii. Napenda kushauri jambo moja kwenye Wizara hii. Kwanza, kuangalia mifumo ya usafirishaji kwenye miji yetu. Ipo miji imekuwa sasa kama ni vigogo vya usafirishaji kwenye mazao yanayotoka kwenye mikoa mbalimbali na yanayotoka kwenye vijiji vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, umeongea kuhusu Mji wa Mbeya asubuhi, lakini mimi nitaongea kuhusu Mji wa Iringa pia. Miji ile inapita au ipo katikati ambapo barabara kubwa zinapita katikati ya ile miji. Tunafahamu katikati ya miji mikubwa kama ile, kuna shughuli nyingi za kibinadamu zinafanyika. Sasa wenzetu hawa ni wataalam, walipokuwa wanajenga miundombinu ya barabara hizi, wakifungua mikoa mingine walijua kabisa geti kubwa litakuja kuwa ni Iringa; walijua barabara kubwa itakayosafirisha magari makubwa yote kutoka kwenye mikoa sita inayotegemewa kulisha nchi hii kwenda kaskazini na Kanda ya Ziwa mikoa sita itapita katikati ya Mji wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walijua kabisa kwamba nchi zile ambazo ni landlocked countries, kwa mfano Zimbwabwe, zinapita katikati ya Jiji la Mbeya. Kwa hiyo, ilitakiwa wenzetu hawa watusaidie kutengeneza miundombinu ya kufungua yale majiji yasiwe barrier. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii viazi vinatoka Songwe vinaozea Mbeya, au vinaanza kuungua Mbeya; vikifika Iringa vinataka kupita vije Dodoma viende Mwanza, vinafia Iringa. Kwa sababu miji haipitiki. Ni sawa na umetengeneza barabara ya njia sita halafu unakwenda kuipitisha kwenye daraja la mita moja, lazima uvunje lile daraja; na ndicho kinachofanyika kwenye miji yetu. Mle kwenye miji ndiyo maana sasa kumekuwa na matatizo. Sisi Wabunge tumeongezewa kazi nyingine nje ya ilani kwenda kuanza kuzuia migomo inayotokea katikati ya vyombo vinavyopita kwenye miji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, umeongelea mgomo uliotokea Mbeya; wiki iliyopita sisi Iringa tulikuwa tuna mgomo wa watu wa barabara, bajaji na bodaboda. Sasa hivi ninavyoongea, kuna vijana wengine pia wamegoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunafahamu, nami nawaomba Waheshimiwa Wabunge, mchawi bwana mkabidhi mtoto akulelee. Mimi nafikiri sasa TARURA tuwakabidhi hawa hawa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, iwe chini yao na wawe na full mandate ya kui-control TARURA ili sasa kule kulaumiana kwamba hapa alitakiwa atengeneze TARURA, kusiwepo. Wasimamie wenyewe kuanzia juu mpaka chini ili wanapofika kwenye mji ule waweze kuwasiliana na wenzao wa TARURA waangalie ni namna gani sasa mji huu tunaufungua? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Iringa tuna bypass. Tunapoongelea miji hii mikubwa, kwa mfano pia Songea kuna bypass, Mbeya kuna bypass. Sasa hizi bypass waliziweka kabisa kitaalam, wamelipa fidia, wamefanya kila kitu, yaani kinachotakiwa ni kuzijenga. Kwa mfano, Iringa tuna kilometa 7.3, ili tuchepushe yale magari makubwa yapite pembezoni activities nyingine katikati ya mji ziendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo tunakuja kwenye ile sifa nyingine ya kupunguza unnecessary traffic flows kwenye miji. Hizo ni unnecessary, tungekuwa tumejenga zile bypass tusingekuwa na sababu ya magari kuja pale. Njegere za akina mama zinaozea kwenye barabara, viazi vya vijana wetu…

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Twaha Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimpe taarifa mzungumzaji kwamba tatizo hilo la kutoweza kuzijenga barabara kwa wakati kama mifano tunayopewa ya barabara ya kutoka Mbeya kwenda Tunduma na barabara nyingine za Iringa, barabara ya Kibiti mpaka Mloka, hii yote ni kutokana na sababu ya mambo ya utelezi. (Kicheko/Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Msambatavangu, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili. Niseme kwamba huu utelezi ndiyo tunataka utolewe. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bypass zijengwe kwenye miji yetu. Kwa nini tunasema bypass zijengwe? Kwa sababu mijini ndipo huduma za jamii zinakopatikana, watu wetu wanakwenda kupata huduma kule. Watu wanafia barabarani. Pia mijini ndiko kwenye masoko. Wewe umefikisha bidhaa mpaka stendi inashindwa kufika sokoni kwa sababu tu ya traffic jam. Sasa uangalie, huo ndiyo utelezi tunasema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, angalia Mji kama Iringa, kwanza barabara yenyewe ya Tanzam inapita iko kwenye mlima, malori makubwa yote yanakwama pale. Lori likianguka katikati pale, Iringa haipitiki kwenda chini, kwenda juu; na malori ya dagaa zilizotoka Mwanza zinaozea pale. Tunawaomba wenzetu waangalie haya, tunaomba sana watusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ninachotaka kuongea hapa, sisi tumepitisha hapa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Sasa inaonekana kama Mpango tunaoupitisha hauendani na mipango ya Wizara nyingine. Nilimsikiliza Katibu Mkuu Kiongozi wakati anaapa, alisema kazi yake ni ku-coordinate hizi Wizara. Tunaomba kupitia Bunge hili aka-coordinate mambo ili Mpango wetu wa Miaka Mitano uende sambamba na mipango ya hizi Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunataka sekta ya utalii ichangie watalii wafike milioni tano ifikapo 2025, na share kubwa tunategemea kupata kwenye utalii wa Southern Zone. Leo tumeiwekea barabara inayokwenda National Park kujenga kwa usawa wa kilometa 1.5, barabara ya kilometa 104, hivi tunapomaliza huu Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2020 - 2025 ni kweli tutakuwa tumefikisha sisi kuchangia pato hilo la Taifa, kufika dola bilioni 6.0? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine tunajiuliza hii mipango tumeweka Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano halafu bado tunaongelea kuunganisha madaraja tu hatuongelei barabara zile zinazokwenda kwenye strategic areas. Tunaongelea kilometa mbili, kilometa tano kwenda kwenye miradi ile ya kimikakati ya kutuongezea pato la Taifa. Je, tupo serious? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana ndugu zangu tuwaangalie Watanzania kwa jicho la huruma, tuwaangalie hawa vijana wetu wa bajaji, wa bodaboda waliopo mijini kwa jicho la huruma. Askari wanafanya kazi kubwa yaani mpaka wanashindwa sasa. Leo TARURA inapewa fedha ya maintenance tu, asilimia 80 mpaka 90, lakini kwa maana ya miradi ya maendeleo wanapewa asilimia 10 mpaka 20. Miji yetu inakua, Waheshimiwa Wabunge tunaposema maintenance maana yake unapewa fedha za kutunza barabara tu zilizokuwepo, hawapewi pesa ya kuongeza mtandao wa barabara. Miji yetu sisi inakua, Iringa TARURA haijapewa fedha ya miradi ya maendeleo na mji unakua wale watu kule wanafuatwa vipi. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, hizi bajaji sijui bodaboda zinafikaje kule kwenye makazi ya watu? Kama watu wanapewa fedha ya kutunza barabara ambazo hazipo, mtoto huyu akabidhiwe wenyewe, wakabidhiwe hawa Ujenzi na Uchukuzi wamchukue TARURA wakae nae ili yanapotokea matatizo tusilaumu kwamba huyu yupo TAMISEMI, tujue ni wenyewe Uchukuzi asilimia mia wamefeli hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaomba TARURA wapewe, nashukuru wamenipatia milioni 120 kwenye barabara yangu inayopita Kleruu, nayo inatakiwa itengenezwe kwa kiwango cha kokoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kiwango cha kokoto si kiwango. Sasa nashukuru kwa ajili ya hilo lakini niwaombe sana tujaribu ku-coordinate mpango wetu na mambo yetu tuliyoyapanga lakini tujaribu kuangalia hizi by pass kwenye majiji zifunguliwe ili huduma zingine za kiuchumi ziendelee. (Makofi)



Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Niipongeze Serikali kwa mpango mzuri ambao imetuletea. Pamoja na kuipongeza kwa sababu imekuwa ni bajeti ambayo imekwenda kugusa maeneo muhimu sana ya wananchi wetu na kutatua changamoto za wananchi wetu, lakini bado nina mchango katika sehemu tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye suala linalohusu elimu, kwa kuwa ili tuendelee tunahitaji tupate watu ambao watakuwa na elimu bora. Niombe sana katika mabadiliko ya mtaala wenzetu watu wa elimu waangalie na kuzingatia mazingira yetu ya Tanzania na kuona namna gani vijana wetu watafundishwa ili waweze kupambana na mazingira ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia na elimu yetu imekuwa nadharia sana, sio ya vitendo. Watoto wanakaa darasani muda mwingi sana, hawana practical, kwa hiyo wanapotoka inakuwa ni shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipo kipengele cha ujasiriamali, ni cha muhimu sana, mtoto lazima ajifunze kuwa ana maono au ana vision tangu kwenye elimu ya msingi. Kwa hiyo lazima tuangalie namna gani tutaingiza kipengele hicho kwenye elimu yetu ili tuwe na watoto wenye mipango kuanzia wadogo watengeze road map ya maisha yao kuanzia shule ya msingi mpaka watakapomaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno niende kwenye suala lingine linalohusiana na masuala ya miundombinu, leo tunajadili bajeti ya Serikali, lakini zamani wakati Taifa letu linaanza kwenye nchi hii tuliwahi kuwa na program ya vijiji vya ujamaa. Nia ilikuwa ni kusogeza huduma karibu na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii katika mipango yetu ya ardhi hata tunapokuwa kwenye shughuli zetu za kisiasa kutafuta kura, unaweza ukaona kwamba tumeacha sasa ile program atuangalii ni namna gani tunawapanga watu wetu kwa makazi na namna gani tunaigawa ardhi yetu kwa ajili ya masuala ya kilimo na kazi zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanaondoka, anakwenda anahamia kwenye mlima alikuwa mwindaji, anahamia huko analeta na mke wake na watoto wanazaliana wako mbali juu ya mlima na hakuna mamlaka yeyote iliyowaambiwa jamani hapa sio sehemu ya makazi, mrudi mkakae na wenzenu. Hii inazidi kutuongezea gharama na ndio maana sasa kumfuata yule mtu ili umpelekee huduma ya barabara, maji, afya ni mbali, yuko mbali na wenzie lakini tayari anataka kupata huduma kutoka kwenye Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweka bajeti ya kujenga barabara kumfuata mtu au kuwafuata watu 600 ambao wako mbali, unatumia zaidi ya bilioni sita au nane na wale watu wamekaa kule wanalima mbogamboga, ukiangalia return kiuchumi pale ni hasara. Kulikuwa kuna sababu gani hawa watu wajitenge na wenzao waende mbali wakaishi peke yao, wakati wangeweza kuishi na wenzao, tukaweza kuwahudumia vizuri pale, wakiwa wamekaa pamoja. Kwa hiyo tunaomba wenzetu hawa wa ardhi waliangalie hilo na mipango yetu iwe hivyo makazi lazima yaimarishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, duniani hawafanyi mambo mapya ila wanafanya mambo yaleyale katika ubora zaidi. Leo hapa tumevaa nguo lakini ni sawa tu na Adam na Eva walivyokuwa wanavaa nyasi, wao walivaa nyasi direct, magome ya miti na walivaa ngozi moja kwa moja, lakini sisi tunavaa ngozi zilizokuwa processed, vinakuwa viatu. Leo tunavaa magauni kutoka kwenye mimea ya pamba. Hicho ndicho tunachosema hatukutakiwa kuacha zile program za Vijiji vya Ujamaa, lakini kuitengeneza ile program iwe ya kisasa na kutusaidia zaidi kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, point yangu nyingine naomba leo kidogo tukumbushana na maneno ya Mungu humu ndani. Kwa sisi wa kristu wenye biblia ya Isaya 32 mstari wa 17 unasema: “Haki kazi yake duniani imetumwa kuleta amani, haki kazi duniani imetumwa kuleta utulivu na matumaini.”

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ndio kazi kubwa ya haki tunaomba sana wenzetu hawa walioko Serikalini, tunapoongea watusikie na wafanyie kazi. Yapo mambo waliyofanyiwa Watanzania wenzetu kwenye nchi yetu hayana tija na yamewajeruhi na hayana tija kwa maendeleo na mustakabali wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, tumeongelea sana hapa maduka ya kubadilisha fedha za kigeni. Wenzetu wale wengine ukiangalia ni wajane, wenzetu wale wengine ukiwaangalia walianzisha zile biashara baada ya kupata viinua mgongo vyao, wengine walianzisha zile biashara mitaji waliipata kwa shida. Ni kweli kama Kamati ya Kudumu ya Bunge inavyosema katika Sura ya 56 ya bajeti yake na mapendekezo yake, kile kipengele cha 8.4, kwamba kulikuwa na lengo la Serikali la kuhakikisha kwamba haya maduka ya kubadilisha fedha za kigeni yanafuata sheria za Serikali na kanuni za Benki Kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, operation iliyofanyika kwenye yale maduka, watu hawa bado hawakutendewa haki, tunaomba haki itendeke kwa sababu mwenye kuhukumu kwenye suala la haki ni Mwenyezi Mungu. Nchi yetu tumejipambanua sana kwamba tunamtegemea Mungu na hatuna ubishi kwenye hili. Ni kweli Mwenyezi Mungu ametusaidia na tumeona alivyotupigania hata wakati wa janga la corona, sasa basi sisi kama viongozi tufanye hiyo practice kwa matendo, kama tunamheshimu Mungu tuheshimu na watu aliowaumba sisi tuwaongoze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwatendee haki wale watu wanaolia kwa ajili ya vitu vyao walivyochukuliwa, fedha zao zilizochukuliwa, mali walizochukuliwa warudishiwe. Wenzetu TRA tunawaomba sana, wakati fulani unakuta Mheshimiwa Rais namshukuru sana, kwa sababu alitoa kauli mwenyewe, kwamba kweli tunahitaji kodi, lakini hatuhitaji kodi ambayo ni ya dhuluma. Tunahitaji kukusanya mapato, lakini hatuhitaji ya dhuluma ndani yake. Tukusanye mapato ambayo hata tunapokwenda kumwomba Mwenyezi Mungu atusaidie, atatusikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunaomba wenzetu wa TRA kwanza wawe wanaelewa, leo hii Mheshimiwa Rais anatoa kauli kwamba sasa kodi zote za miaka ya nyuma, miaka sita au saba iliyopita jamani basi, ukienda TRA ndio kwanza wanatoa demands note za kuwadai watu kodi miaka nane au tisa iliyopita. Unawauliza hili likoje, wanakuambia sisi tupo tunafuata maelekezo na sheria, ni kweli kauli ilitolewa kisiasa, lakini sisi tunafuata mwongozo, tunataka maelekezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Rais anapokuwa anatoa, ameshafanya uchunguzi wa kina, kwa sababu yeye ana milango mitano ya fahamu ana vyombo vimeshamsaidia mpaka anafikia hatua ya kutoa tamko. Kwa hiyo wenzetu wafuate mambo ambayo tunawaambia tutende haki kwenye Taifa letu, tuwatendee haki, hii iendane na kesi zingine za biashara. Wapo wafanyabiashara wengi waliofanyiwa vitu vingi ambavyo havikuwa sahihi. Tunaomba sana kero zao zitatuliwe kesi zao na mashtaka yao yaangaliwe kwa kina ili kama kuna uonezi wowote uliofanyika, watu hawa waweze kusaidiwa na warudishwe kwenye hali ya kawaida ili tuendelee kujenga imani kwa wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la elimu, tumejipambanua kwamba elimu yetu haina ubaguzi na mimi hapa naomba niseme tumesema tunataka Watanzania washiriki kwenye uchumi, lakini wapo wawekezaji waliowekeza kwenye nchi hii kwenye sekta ya elimu, wamejenga shule, wamejenga vyuo, lakini namna ambavyo wakati mwingine tunawachukulia, hatuwachukulii kama ni watu ambao wanatusaidia kama Serikali kutoa huduma kwa jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuwachukulie kama ni watu ambao wamechukuwa nafasi ya Serikali kuwahudumia wananchi na wao wana-feel gap ya kutoa elimu kwa wananchi. Kwa hiyo suala la kutoa elimu bure, tuwasaidie basi hata hawa private pamoja na kwamba wao au shule binafsi wanachaji ada, leo Serikali inashindwa nini hata kuwachangia gharama za mitihani tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wale ni Watanzania wanaolipa kodi na walikuwa na haki ya kusoma kwenye public schools au kwenye shule zetu za Serikali, lakini wameamua kusomesha watoto wao kwa gharama na ndio walipa kodi wazuri wa nchi hii. Kwa nini leo shule ina wanafunzi 10 kwa sababu haijafikisha wanafunzi 35 inatakiwa ilipie wale wanafunzi 25 ada za mitihani hata kama hawapo. Kwa hiyo, katika nchi hii bado tuna malipo hewa kwenye elimu, imefanyika michakato ya wafanyakazi hewa, lakini sisi kwenye sekta ya elimu na Wizara ya Elimu bado watu wanalipa ada za mitihani hewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikisema hivi namaanisha kwamba, ikiwa huna watoto 35, una watoto 10 unachajiwa fedha ya watoto 35. Hawa watu wanawekeza return on investment kwenye elimu inachukua miaka 10, ndio mtu aanze kupata faida kwa hiyo tunawaomba wenzetu wa Wizara wajue hawa ni partners wetu, hawa ni Watanzania, wamewekeza kwenye elimu, tunaomba wasaidiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyaraka za elimu pia ziangaliwe. Tuna tatizo kubwa sana tunaweza kuona la kawaida, leo tunatangaza shule zote zitafunga tarehe 30 mwezi wa Sita, tunaomba tuulizane maswali, je, miundombinu ya kuwasafirisha wale watoto wetu kutoka kwenye mashule kwenda kwa wazazi wao tuna uhakika ipo?

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna changamoto kubwa unakutana na watoto wamelala stendi, Mbunge unapigiwa simu sijui watoto wa shule gani wamekosa basi wamelala stand au mabasi ndio yametolewa mabovu wakati ule, wamepakiwa watoto wetu wanalala njiani unapigiwa, usalama wao unakuwaje? Kwa sababu mabasi yanayotumika ni yale yale ambayo siku zote ndio yanasafirisha abiria. Yakitoka mengine ni mabovu kwa sababu hakuna mtu atakayenunua basi asubiri tu msimu wa shule kufunga asafirishe tu wanafunzi. Kwa hiyo watu wa wizara tunaomba watusaidie katika waraka mbalimbali wanazozitoa na maelekezo wanayoyatoa, basi wawe wanaangalia na mazingira na hali halisi ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno haya, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango duniani ni mpango kama ilivyo mipango yote na ina sifa zake. Tumeletewa mpango na tumeusoma na taarifa yake na jinsi ulivyo. Mpango huu una chanzo chake ambacho ni Ilani ya Chama cha Mapinduzi; na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ni mkataba kati ya Watanzania na Serikali wanayoenda kuiunda na mambo ambayo wanategemea kwamba Serikali itakwenda kuwafanyia. Serikali ni Mkandarasi ambaye amepewa tenda na CCM kutekeleza yale ambayo iliahidi kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mipango iweze kutekelezwa lazima kuwe na malengo. Malengo tumejiwekea na tunayaona yapo kwenye mpango, lakini Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inatambua kabisa kwamba, Mpango huu ndio unakwenda kutekelezwa katika ule Mpango wa Miaka Mitano ambayo tumeupitisha, ambao ndio unakwenda kutimiza dira ya maendeleo ya Taifa ambao tumeanza kutekeleza tangu mwaka 2000 mpaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa basi, ninachoona shida kwenye Mpango wetu ile kutokuwa unasomana na ule Mpango Mkuu wa Miaka Mitano kwa sababu malengo yake kama tunasema kwamba, mpango wote unatakiwa kuwa na malengo yanayopimika, yanayokuwa na muda maalum, yanayoweza kufikika, maana yake kuna sifa za malengo. Mpango huu kuna mambo ambayo ukiangalia katika miradi yetu ya maendeleo tumeweka malengo kwamba tutakuwa na miradi ya maendeleo ambayo itakwenda kuchochea ukuaji wa uchumi ambayo ni ujenzi labda wa barabara. Barabara hizi zinakwenda kufungua fursa za kukua kwa uchumi, halafu barabara zile hazijawekewa muda lini zinakwenda kukamilika. Maana yake ni kwamba, yale malengo hayasaidii mpango huu wa muda mfupi kufikia mpango wa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tuna barabara inajengwa kuanzia Itono – Ludewa kwenda Manda, kilometa 211. Serikali inasema barabara hii imeanza ujenzi na ujue tupo kwenye utekelezaji wa Mpango huu wa Miaka Mitano, maana yake tuko mwaka wa tatu. Tumeanza ujenzi wa kilometa 50 kuanzia Lusitu mpaka Mawengi na umekamilika kwa asilimia 95. Sasa swali langu ni hili hapa, huyu mkandarasi kapewa kazi ya kujenga barabara hii kwenye Ilani ya CCM yenye urefu wa kilometa 211. Anatupa kukamilika kwa kipisi cha kilometa 50 kwa asilimia 95 ina maana gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo hajatuambia hizi asilimia 161 zinazobaki atakamilisha katika hii miaka miwili iliyobaki. Hapa ndipo kunakuwa na tatizo la mpango na tusipowekana sawa maana yake ni kwamba, tutakuwa tunaweka hii mipango halafu haitimii. Sasa tumeshamaliza dira ya maendeleo ya miaka 25 na Serikali ya CCM inaitambua hiyo na imeeleza kwenye ilani kwamba, itaisimamia Serikali yake kuhakikisha inaandaa mpango mwingine wa dira ya miaka mingine 25, maana yake itakwenda mpaka 2050.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najaribu kuuliza kama hatutawekeana malengo kwamba, ninyi mwaka huu mkiingia katika hii barabara jengeni kilometa 40, mwaka unaofuata tutajenga kilometa 42, mwaka unaofuata tutajenga kilometa 42, mpaka miaka mitano tufikishe zile kilometa 211 hii mipango yetu tutakuwa tunafikiaje? Kama watu watakuja tu ofisini, sisi tumejenga kwa asilimia 95 kilometa 50, ndizo ulizotumwa? Wewe umetumwa kutengeneza kilometa 211, tuambie hiyo asilimia uliyojenga katika hiyo kilometa 211, usituambie katika hizo ulizoamua wewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sawa na unakwenda kumkagua mkandarasi mradi, halafu anakwambia nimekamilisha kwa asilimia 90 kipande hiki, wakati wewe unajua kipande kile ni kidogo sicho ulichompa. Kwa hiyo, tunataka mpango unaokuja sasa uwe una time ya kutuhakikishia kwamba, hizi barabara tunazosema zinafungua uchumi wa Taifa letu katika miaka mitano zinaishaje? Kwa mwaka wa kwanza zinajengwa kilometa ngapi, ngapi, kwa miaka inayofuata mpaka tutakapofikia kwenye zile ambazo tunajua kabisa kwamba, ndani ya miaka mitano tutakuwa tumekamilisha ile barabara yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaendelea kujenga hizi barabara kwa kilometa moja, kilometa mbili, tunafungua uchumi. Kwa mfano, barabara ya Iringa MR mpaka Itunundu kilometa 70, kila siku wanajenga kilometa moja moja miaka 70 watakua lini kwenda kwenye uchumi wa kukua kwa asilimia nane na watu watakuwa answerable vipi? Yaani unamuulizaje mtu kwamba, wewe Wizara yako ya Uchukuzi imefanya kazi nzuri kama hukumwekea lengo kwamba, lazima barabara hizi zinazofungua uchumi ujenge kwa asilimia 40 au 50?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndio kwenye shida ya mpango. Kwa hiyo, mipango tunayokuja nayo huku mbele ifanyiwe mapinduzi tuambiwe barabara hii uliyosema unaijenga kwa miaka mitano umejenga kilometa ngapi? Nimejenga kilometa 150; hizi zilizobaki unamaliza ndani ya hii miaka miwili iliyobaki na kama hujamaliza kwa nini? Hapo ndipo tutakuwa tunakwenda sawa na mipango mingine yote duniani, lakini tukienda hivi itakuwa kama ile michezo ya kuchezea vile viberiti chekundu cheusi, chekundu cheusi, kila mtu atakuja atatuambia hapa sisi tumejenga kilometa mbili kwa asilimia 90. Kilometa mbili kwa asilimia 90 out of kilometa ngapi? Haya ndio maswali ya kujiuliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine kikubwa ambacho kipo kwenye huu Mpango; pamoja na kwamba tunakusanya fedha, udhibiti wa fedha zetu umeendelea kuwa weak. Tumeelekeza sana kelele nyingi kwamba, Serikali za Mitaa ndiko fedha nyingi zinakopotea, lakini iko miradi hapa ambayo imewekwa na Wabunge wengine wameisema na yenyewe inapoteza tu fedha za Serikali, haina tija. Katika karne hii kuipatia taasisi fedha, unaipatia taasisi fedha bilioni moja, inakwenda kufanya ubunifu na ndio wanasema inakwenda kuwa ni kitivo cha kubuni zana za kilimo vijijini kama CARMATEC, unaipatia bilioni moja, inakuja imekutengenezea mikokoteni ya kuvutwa na ng’ombe nane. Imetengeneza sijui mashine za kubangua korosho mbili, huu ni utani wa uwekezaji kwa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu ambao tunatumia gharama kubwa tumewekeza, tunawafundisha, tunawapa mafunzo, especially vijana. Tunawapeleka katika majeshi, kwa mfano JKT, wanafanya kazi kubwa sana ya kuwafundisha wale vijana uzalishaji mali, uhodari, ushujaa na wale wanaweza kufanya kazi popote. Wao JKT lengo lao la kuanzisha si kwamba kutoa ajira kwa vijana, lakini sisi Serikali ya CCM imetutuma kuandaa ajira milioni nane. Hawa vijana wanaangaliwa vipi? Wanaachwa vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unamwachaje mtu ambaye umesham-train anaweza kufanya kazi, anaweza kulima, anaweza kutengeneza, anaweza kupambana na mazingira ya Kitanzania, kulala popote akaweza kulima, akafanya nini, ukamuacha kama kijana wako, kama nguvukazi, kumwendeleza na wakati umeshatumia gharama kubwa ya uwekezaji kwake. The same applies tunafanya kwa watu tunaowasomesha, tunafanya kwa vijana ambao wanamaliza vyuo vikuu, hatuna mpango kabambe kwamba, vijana wamemaliza, hawa wana elimu hii, vijana hawa wamemaliza SUA wana elimu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunahangaika mpaka vijijini; China waliamua kwa pamoja wakasema sasa tunachukua vijana milioni tano, tunawapeleka vijijini na wengine tutawapeleka nje ya dunia wakajifunze namna ya kufanya kazi. Hawa nao waende vijijini kule, wakakae na wanakijiji, waangalie wanafanya nini, halafu watupatie njia mbadala za kufanya mambo wanayofanya kisasa zaidi. Sisi tuna mpango gani kwa vijana wetu na hizi milioni nane? Hizi ajira milioni nane tulizopewa na chama? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali watu na rasilimali vitu hatuweki vizuri. Leo tuna LNG, mradi wa gesi, taarifa imekuja hapa kwamba, mradi ule wa gesi tumejenga barabara kuzungushia eneo lile, ndio kazi zilizofikiwa kwa bilioni nne karibu na. Tumezungushia barabara kwenye ule mradi, halafu mambo mengine yaliyofanyika kwenye mradi ule tunaendelea na utafiti wa kisayansi, tunaendelea na utafiti wa kuweka mipango, sasa kipi kinaanza kati ya kuku na yai? Unaanzaje kujenga barabara na kuzungushia eneo ambalo bado unaendelea kufanyia utafiti wa kisayansi, hujajua kwamba, utatakiwa uweke mitambo ya kiasi gani? Kwenye hizo barabara hiyo mitambo itapita au haitapita?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante. Kengele ya pili.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba Mheshimiwa Waziri akija hii miradi mingine ambayo haina tija aitoe na taasisi ambazo zinachukua hela hazina tija zitolewe. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi pia niungane na Wabunge wengine kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungnao wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya katika Taifa letu na hasa kwa kuangalia wananchi wetu wa chini kuhakikisha kwamba anashughulika zaidi na masuala ya elimu na afya na tumeona kwa vitendo siyo kwa maneno. Nimtie moyo kwamba tupo nyuma yake na tutaendelea kupigana na kuhakikisha kwamba kazi inaendelea na zaidi sana kwa kuwa amesimama kama taa ya mabinti zetu na sisi wanawake tutahakikisha haizimi, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitakuwa naongea mambo mawili na hayo yote yanahusu ukatili. Jambo la kwanza nitaongelea ukatili wa kijinsia lakini dhidi ya watoto, lakini nitaongelea pia ukatili wa kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa leo tumekaa hali ya watoto wetu kwenye Taifa hili si salama hata kidogo. Mheshimiwa Waziri amesema hapa kati ya mashtaka yaliyopelekwa mahakamani ya ukatili wa kijinsia asilimia 33 ni kwa ajili ya watoto na 67% ni kwa wanawake. Lakini nimuongezee hajasema wanaume, lakini upo ukatili pia dhidi ya wanaume na tafiti zinaonesha kabisa kiwango cha wanaume kupigwa kimeongezeka mpaka 71.7% wakati wanawake wamepigwa kwa 73.5%. Ukichukua takwimu hizo zinaonesha wanaume wanashuka kwa sababu wao walikuwa juu zaidi kwenye kiwango cha kupiga na wanawake wanapanda kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu hizi zote zinaonyesha namna gani sasa athari inakwenda kuangukia kwa Watoto, kwa sababu vipigo vinavyoendelea usitahimivu wa ndoa unakuwa haupo, watu wanaachana wanaacha watoto katika hali hatarishi. Katika hiyo 33% watoto wa kiume waliofanyiwa ukatili ni 11.5% na watoto wa kike ni 22%. Tunaposema watoto wa kiume wamefanyiwa ukatili wa kingono maana yake wameingiliwa kinyume cha maumbile. Ipo miaka kumi inayokuja usishangae kuona mtoto wako wa kiume anakuja nyumbani na mkwe wako wa kiume na tusije tukaanza kuleta maneno astaghfilillah, tusije tukaanza kuleta maneno God for bid, tusije tukaanza kuleta maneno Mungu niepushie mbali, atakuwa hajakuepushia mtoto wako wa kiume, atakuwa amekuja na mwanaume mwenzie na anataka kumuoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu katika watoto waliofanyiwa ukatili 3% ndiyo waliopata ushauri nasihi na kutibiwa, 7% wako mitaani na wale wanageuka kuwa makonki master na watoto wa kike 13% tu ndiyo waliopata ushauri. Nasema hivi kwa sababu sisi Iringa tumepata tatizo hili, mtoto mmoja ambaye ameweza kuwalawiti wenzie 19 ndani ya mwezi mmoja, sasa wale saba wanaobaki ambao hawajafanyiwa matibabu wala ushauri nasihi wanarudi mitaani na wanaendeleza ile tabia. Nilivyoongea na yule mtoto aliniambia kwa uchungu sana akaniambia nilifanyiwa matendo haya nikiwa nursery school miaka mitano, leo hii tumepata takwimu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri watoto walioandikishwa nursery school ni karibu 1,198,564 lakini watoto walio nje ya shule kwa maana ya pre-primary kwa data zilizoko na utafiti ulioko wa UNICEF ni 61.8%. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujaona mpango hapa tumesema tumewaandikisha hawa ni awali na tunapongea awali hawa ni watoto wa shule ya msingi miaka sita chini ya hapo wako nyuma na yule mtoto anasema alifanyiwa akiwa chini ya miaka sita.

Leo aliachwa amekwenda mtaani na akaniambia Mheshimiwa Mbunge nikasema nikusaidiaje kama Mbunge wako maana mtoto ana miaka 13; akaniambia naomba uhamishe watoto wote wanaokaa lile eneo uwapeleke shule ya bweni au uwapeleke kwenye vituo maana yake pale watoto wote ndiyo tunachofanya.

Sasa nikawa nasoma pia maendeleo ya wenzangu Wizara mpya ambayo mama ametuanzishia ya Maendeleo ya Jamii, wanasema wameanzisha kamati za kulinda watoto na wanawake. Kamati 18,186 kati ya kamati 20,750 walizotaka kuanzisha kwenye nchi hii kwa ajili ya kulinda wanawake kwenye mitaa na vijiji, kamati hizo hazipo na hazifanyikazi, hatujaziona. (Makofi)

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Jambo hili la ulawiti kwa watoto wadogo, ukatili wa kijinsia kwa Watoto, limeshika kasi sana katika nchi yetu na kumekuwa na kesi nyingi sana ambazo mwisho wake haueleweki kumekukuwa na rushwa mbalimbali na hakuna hatua madhubuti ambazo zinachukuliwa mimi niombe sasa kupitia hili kwamba Mheshimiwa Mbunge anachokisema ni sahihi kabisa na wale wote watakaobainika basi wahasiwe iwe ndiyo adhabu kubwa ikiwa ni pamoja na kifungo, ahsante.

NAIBU SPIKA: Taarifa hiyo?

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kasoro ile ya kuhasiwa. Sipokei ya kuhasiwa kwa sababu tuna namna tutawashughulikia na kuwashughulikia hawa kwa sababu zipo sababu zinazosababisha wafanye mambo haya ikiwepo ukata, nitaongezea yaani yale mambo ya uchumi yale.

Sasa hivi mapenzi au huduma ya mapenzi ni product kama product zingine watu wamepunguza purchasing power hawana nguvu ya kununua kwa hiyo wanakwenda kwenye kundi la watoto wadogo na kuwaonea. Kwa nini wamepunguza purchasing power? Ni kwa sababu ya ukatili mbalimbali unaofanyika kwenye jamii kiuchumi ikiwepo pamoja naweza nikasema sasa hivi na sisi tunachangia kama kuna Wizara hapa inafikiria kutowapa kipaumbele Watanzania katika miradi inayotolewa na Serikali hao ndiyo wanaosababisha matatizo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukiniambia nguzo za umeme zitanunuliwa nje ya nchi una maana vijana wangu wote walioko Iringa, Songwe, Tanga wote wamepanda miti wakose fedha, watakapokuwa wanahitaji la mapenzi watafanya nini? Kwa sababu kiuhakika sasa hivi hamna mwanamke atakupenda sura kwa sababu wanaume kwanza hawana sura nzuri unampendaje mwanaume sura. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanamme anapendwa kitu alichonacho anapendwa fedha leo tunapoharibu mazingira ya utendaji kazi wa machinga hatuangalii kama mimi Mheshimiwa Bashungwa Iringa hujanipa hela yoyote ya kuandaa mazingira ya machinga. Wanakaa katika mazingira hatarishi wanapoteza mitaji wale ni watoto wa kiume rijali unategemea unaenda wapi? Inapofika hatua anataka hamu ya mapenzi anafanyaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ndiyo tunayoyasema, lakini pia kuendelea kuwanyanyasa vijana wetu waliojiajiri kwa mfano kwenye bodaboda, kwenye bajaji wanafanya kazi zao unawabana unawanyanyasa kwa leseni wasifanyekazi vizuri una mnyanyasa yule kijana akikosa hela atafanya nini? Huo ndiyo unyanyasaji wa kiuchumi.

Sasa tuhakikishe kwamba Watanzania wanajengewa mazingira mazuri ya kufanyakazi, wanajengewa mazingira mazuri ya tiba, mimi naomba vijana wangu pale watibiwe vizuri zile hela za vijana naomba jamani kutoka mfuko wa Waziri Mkuu shilingi milioni 200 tu tukawawezeshe vijana wa pale wafanyekazi wawe na uwezo wa purchasing power za mapenzi, wasibake watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana tuangaliwe masuala ya huduma za afya tuboreshe, watoto hawa wengine wanabakwa wamekosa nimekuambia ni asilimia tatu katika 11 wanaopata matibabu lakini hata wakienda hospitali sisi tumetoa watoto wengi kuwapeleka Muhimbili pia wakatibiwe baada ya kuwa wamefanyiwa ubakaji hatuna Hospitali ya Wilaya na leo sioni kama imetengwa hapa nimetengewa milioni 500 tu ya kukarabati lakini tuliwaomba tujengewe kwa sababu ile iliyokuwa ya Wilaya mmechukua Mkoa na inahudumia mkoa mzima tunaomba hospitali yetu ya Wilaya ili sisi watoto wetu waweze kutibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme hivi katika masuala ya ukatili haya mimi nasimama leo kama Mheshimiwa Mbunge hapa kwa sababu kuna masuala ya ushirikina yapo ndani yake, sasa ushirikina ni mambo ya rohoni na tunayashughulikia kiroho. Walioko humu ndani watumishi wa Mungu watanielewa, mimi nasema hapa sasa kama Mbunge na ninyi wenzangu kama mnaniunga mkono mtajibu amina mwishoni nasema hivi Mungu tusaidie hatutawafanyia hatutawahasi kama alivyosema Mheshimiwa lakini ninaomba hivi tuachilie nguvu za Mungu kuanzia hapa zikawashughulikie wote kwenye kile kiungo wanachotumia kulawiti watoto wetu, kipigwe nguvu kisifanye kazi na zile mashine mbili zinazozalisha nguvu, zipotee kabisa na madaktari watakapoona mtu mwenye dalili hizo mnitafute ili tumuombee arudi katika hali ya kawaida na tumfanyie counselling ili watoto wetu waendelee kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye masuala ya kiuchumi tuwatengenezee vijana wetu mazingira rafiki ya kufanyakazi tusiwanyanyase mama ntilie sijui akina nani wanapoonekana wanafanyakazi usimwage bidhaa zao, uangalie namna utakavyotumia hekima kuwasaidia ili wajijengee uchumi. Tumesema hapa tuwape vipaumbele Watanzania kwenye miradi tuwape vipaumbele tuwape elimu ili Watanzania waweze kuwa na purchasing power ya mahitaji yao ya muhimu ikiwepo suala la mapenzi, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie. Kwanza nichukue nafasi hii kupongeza sana Ofisi ya CAG kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha kwamba Bunge hili linakwenda siyo kama kipofu, bali tunakwenda huku tukiwa tunaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo ambayo nataka niongee kutoka kwenye ripoti ya CAG, nami ni Mjumbe wa Kamati. Kwanza kabisa, yapo mengi ambayo Waheshimiwa Wabunge wameshaongea. Cha kwanza nilichotaka kuongea ambacho CAG amekiongea na kinaonesha wasiwasi, nami binafsi pia nikapata wasiwasi, kwanza ni kuhusiana na fedha za ruzuku ya maendeleo ambazo zinapelekwa kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, CAG anasema pesa za maendeleo zinazopelekwa kwenye Halmashauri zetu baadhi yake zinaonekana zimepelekwa bila kupitishwa au kupatiwa idhini kutoka kwenye Bunge hili. Wasiwasi wangu unaanzia hapo. Zipo zaidi ya Halmashauri 19 ambazo zimepelekewa fedha zaidi ya shilingi bilioni 47 bila idhini ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi yetu kubwa hapa kama Wabunge ni pamoja na kuisimamia Serikali na kupitisha hizi bajeti za Serikali. Sasa nashindwa kuelewa, ni kwa nini fedha hizi shilingi bilioni 47 zipelekwe katika Halmashauri, hata kama nia ni njema, ndiyo zipelekwe katika hizi Halmashauri bila Bunge kujua au kuidhinisha matumizi yake kwenye hizi Halmashauri?

Mheshimiwa Naibu Spika, wasiwasi wangu unakuja, pale ninapojiuliza, wenzetu Serikali wana mpango gani na Bunge? Je, wanataka kutunyang’anya ajira zetu? Kwa sababu sisi kazi yetu ndiyo hiyo, tuje hapa tupitishe bajeti, tuwahoji na kadhalika. Sasa unapokwenda moja kwa moja unapeleka fedha hizi bila kunipa mimi, una nia gani? Kwamba unanifuta kazi yangu, au una mpango gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, fedha zimepelekwa kwenye miradi ya maendeleo zikiwa pungufu. Hapa naipongeza Serikali. Zaidi ya Halmashauri 163 zimepelekewa shilingi bilioni 500 kama ruzuku ya miradi ya maendeleo, lakini wamejitahidi kwa sababu upelekaji wa miaka mitano mfululizo ni wastani wa asilimia 46; lakini kwa mwaka 2020/2021 wamepeleka asilimia 62 kwenye ruzuku ya miradi ya maendeleo. Hapo tunawapongeza na tunaona nia njema ya Serikali, lakini bado kuna upungufu wa asilimia 38 zaidi ya shilingi bilioni 300 ambazo hazijapelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaiomba Serikali iangalie namna, kwa sababu tunapopeleka fedha hizi kwenye miradi ya maendeleo ndivyo tunavyokwenda kuchakachua uchumi kule chini kwa watu wetu. Halmashauri tatu zenyewe zimepelekewa fedha kama ambavyo jinsi tulikuwa tume-plan bila kuwa na mambo yoyote meusi ndani yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili; ili tuendelee tunahitaji watu; lakini tunahitaji watu tu, tunahitaji watu walioongezewa thamani. Hatuwezi kuendelea kama tuna watu ambao hawana thamani kubwa. Taarifa ya CAG inaonesha bado yako madai kwa watumishi wa umma wa nchi hii. Wanatudai mishahara shilingi bilioni 63. Yapo madeni ya malimbikizo ya posho, likizo kwa watumishi milioni karibu 96,650,000,000. Hawa ndio rasilimali watu tunaotegemea kwamba wafanye kazi kubwa kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hatutaweka uwekezaji kwa watu hawa, ina maana utendaji wao ndio maana unakuwa ni duni. Watu hawa ndio tunaopelekea mabilioni ya fedha kwenye miradi ya maendeleo, halafu hujampa fedha yake ya nauli anapokwenda likizo, ndio maana unakuta sasa wana-temper na mifumo, wanafanya mambo meusi meusi ili angalau waweze kufidia ule upungufu na makali wanayopata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tumeelezwa hapa, Manispaa moja tu ya Ilemela kwenye mitando tayari wame-temper na shilingi bilioni karibu nane, zimefutwa vocha za karibu 822 kwenye mfumo bila utaratibu unaoeleweka. Tumeelezwa hapa, Ubungo wameingiza figure kwenye mfumo ambao Mwenyekiti wangu wa Kamati amesema tu kwamba ni shilingi milioni 500 ambayo haieleweki yaani. Ukiwauliza, wanakwambia ilikuwa ni namba ya simu. Unashindwa kuelewa, namba ya simu gani inaanza na kodi ya 500? Ni ujanjaujanja na ubadhirifu ili kuhakikisha kwamba wanakuja ku-temper na fedha za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tusipoangalia, na kuwaangalia watumishi wa umma, hatuwezi kufanya mambo makubwa yakaenda sawa sawa na maendeleo kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado kuna malalamiko ya kikokotoo kwenye nchi hii…

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, …

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa mchango wake, lakini nadhani Bunge hili pia linapaswa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sababu baada ya CAG kuwa ametoa taarifa hiyo na hasa kwenye malimbikizo ya mishahara kwa watumishi wa umma; na kwa kuwa Mheshimiwa Rais alishajipambanua kwamba anahitaji rasilimali watu iweze kupatiwa haki na stahiki iweze kutekeleza wajibu sawa sawa; mpaka tarehe 31 Januari, Serikali ya Awamu ya Sita imeshalipa malimbikizo ya mishahara kwa watumishi wa umma 116,792. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haikuishia hapo. Katika hayo malimbikizo ya mishahara imekwishakutumia fedha za Kitanzania shilingi bilioni 199.365. Kwa hiyo, tunampongeza CAG kwa kazi nzuri, lakini hapo hapo pia tumpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuona jambo hilo na kulipa stahiki za watumishi wa umma. (Makofi)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jesca.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba unilindie muda wangu, lakini nashukuru kwa taarifa hiyo ya Serikali na naipokea. Hata hivyo tunayojadili hapa ni ile iliyoishia Juni, 2021. Kama wamekwenda hatua hiyo, tunawapongeza zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwaombe, suala lingine linaloleta malalamiko, pamoja na mambo mengi tuliyoambiwa kuhusiana na kikokotoo, lakini kikokotoo kile ndani ya watumishi wa umma kinasumbua. Tunaomba Serikali ione namna ambavyo itakaa na watumishi wa umma na kuona wanafanya kazi kwa moyo bila kuwa na malalamiko.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kukaa hata na Jeshi la Polisi tu, wakielezea hali yao ya utendaji wa kazi wanakwambia sisi hatuna hata muda wa kupumzika kusema tutatafuta hela ya ziada kwa ajili ya kuweka kibanda. Tunategemea tukilipwa mafao yetu ndiyo tuweke kibanda. Leo ukiniambia unanipa kidogo halafu unanilipa kidogo kidogo unakuwa hunisaidii. Tunaomba Serikali ikakae ili kuendelea kupunguza malalamiko haya kwa watumishi wa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho nataka kuongea, upo ubadhirifu wa mikataba ambayo Halmashauri zetu zinaingia, na uwekezaji ambao Halmashauri zetu zinaingia. CAG ameelezea. Yapo mambo ambayo Halmashauri zinafanya bila upembuzi yakinifu, kwenda kuwekeza miradi ya ujenzi wa mastendi na masoko. Unakuta kwa sababu tu Halmashauri hii imejenga soko, na wengine wanataka wakajenge soko na wangine wanataka wakajenge stendi na wengine wakaige kitega uchumi hiki, lakini bila kuangalia mazingira yao yanaendana na hicho kitega uchumi wanachotaka? Ndiyo maana yapo majengo mengi sana yamejengwa kwa gharama kubwa lakini hayatumiki ipasavyo kwa sababu Halmashauri zetu hazifanyi upembuzi yakinifu wa kujua mradi ule kama unaweza ukawa sahihi kwa mazingira yao na kama watu wao wanauhitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Serikali iwasimamie. Hizi Halmashauri, Wizara husika, isimamie. Ile ya kwamba tunakwenda kujifunza mahali fulani, Waheshimiwa wanasafiri wanakwenda kujifunza mahali, anachukua tu ile utaratibu wa kujenga Machinga Complex ya Dar es Salaam anataka labda ajenge Iringa, wakati ni tofauti kabisa. Yaani Machinga wa Iringa ni tofauti kabisa na Machinga wa Dar es Salaam, na hawawezi kuendana katika biashara zao wanazozifanya. Kwa hiyo, hii imeipotezea Serikali mapato hela nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia zipo taasisi nyingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Haya, nakuongezea sekunde 10.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo taasisi nyingine ambazo nazo zinasababisha Halmashauri zetu kupata hasara. Taasisi kama TEMESA ni za Serikali, lakini nazo zimekuwa funza kwenye Halmashauri zetu. Kwanza, ukitaka kupeleka gari TEMESA watakuandikia vifaa vya bei kubwa kuliko hata kwa Mangi, unakwenda unatengeneza kwa gharama kubwa, wanakufungia kifaa kimekufa, yaani hawaeleweki. Kwa nini tutumie TEMESA kama tunajua kabisa hii inatuletea tatizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna NHIF, kila wakati kwenye hela za vituo vyetu vya afya wanatafuta visingizio vidogo vidogo, kwamba hawa wameshindwa kujaza fomu…

NAIBU SPIKA: Ahsante. (Kicheko/Makofi)

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Mpango wa Tano wa Maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ya msingi tunapotaka kufanya mabadiliko ya kiuchumi na kwenye biashara. Ukichukua mfano wa nchi ya China ilipotaka kufanya mabadiliko yake kwenye masuala ya uchumi na biashara zaidi ya miaka 40 walikuwa wakiendelea kusuguana na sheria na sera zao. Mipango na mikakati yao ilikuwa imekaa vizuri; ilikuwa ikijali muda, lakini ukienda kwenye mambo ya sheria na sera zao zilikuwa zinawarudisha nyuma na zikafanya uchumi wao kuendelea kuwa duni, ulishindwa kuendelea kukua, tegemezi na usiozingatia ushindani wa kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye walipoamua sasa kuanza kubadili sera na sheria zao ndipo walipoanza kuleta maendeleo makubwa na ndani ya miaka nane kwa ripoti za Benki ya Dunia, walikuwa wanakua mara mbili zaidi ya GDP ambayo ilikuwa ni kwa asilimia 9.5. Ndipo walipoweza sasa kutoa umaskini kwa watu wao zaidi ya milioni 800 maana tunapoongelea China ni watu zaidi ya milioni 1,400.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sasa Mpango huu wa kwetu wa Maendeleo wa Miaka Mitano ni mzuri na umezingatia standard na spidi au umejikita katika muda lakini kikwazo kikubwa kitakachokuja kutukuta, katika ukurasa wa tano wa maeneo ya muhimu ya kuzingatia ambao Mpango unaeleza, umeeleza mambo mazuri lakini haukuweka msisitizo katika kuhakikisha kwamba tunabadili na sisi sheria na sera zetu ambazo huwa zinatusababisha tusiende kwa spidi au tusiende kwa wakati ule ambao tumeupanga, hicho kipengele hakijawekwa. Kwa hiyo, tunaomba tushauri kwamba katika Mpango huu tujaribu kuangalia namna gani tutabadilisha sheria na sera zetu ili ziweze kuendana na muda ili tuweze kuutekeleza huu mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi sana tumekuwa tukipanga vitu vingi lakini unakuta kuna sheria zinakinzana. Tunakwenda kwa spidi tunataka kuinua utalii, Mpango unatuambia kwamba tutoke katika watalii 1,500,000 mpaka itakapofika 2025 tuwe tumefika watalii 5,000,000, lakini kuna sera nyingine ambazo zipo sasa zinahusiana na masuala ya kutoa vibali au permit za kuishi, unakuta zinakinzana na ile sera ya sisi kuboresha spidi ya kuendeleza utalii wetu au kuboresha spidi ya uwekezaji. Mwekezaji anakuja katika taifa letu, amekuja na mtaji, anakuja kupambana na Sheria ya Labour ambapo yeye anataka kuja na mke wake lakini sheria inamkatalia asije na mke wake au anapata usumbufu kupata permit ya kuishi na mke wake. Sasa unakuta vitu kama hivi vinakuwa vinakinzana, tusipoziangalia sheria na sera zetu, bado hatutaweza kuutelekeleza huu Mpango kwa wakati kama ambavyo tunatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukajifunza kutoka kwenye Sekta ya Madini, namna ambavyo madini yamechangia kwenye maendeleo yetu katika Mpango wa Pili, ni kwa sababu pia yalifanyika mabadiliko makubwa ya kisheria kwenye sheria za madini na ile ikatusababisha tukaenda vizuri. Kwa hiyo, ushauri ni kwamba tunaomba sheria na sera nazo ziangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua kwamba tuna mkinzano wa kisheria na mipango yetu utaona mara nyingi sana mambo yetu mengi yanakwenda kwa waraka, matamko, yanakuwa kama ya zimamoto hivi. Kwa sababu kama sheria ingekuwa inakwenda sawasawa na mipango, hivi vitu vya zimamoto, kwenda kwa matamko na nyaraka visingekuwa vinakwenda namna hii. Hii inaonesha namna gani sheria yetu inawezekana haiko sawasawa na mipango ile ambayo tunaiweka. Kwa hiyo, tujitahidi kubadilsiha sheria zetu na tujitahidi kuangalia mabadiliko makubwa kwenye sera zetu ili tuweze kwenda sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wetu unatakiwa ujengwe sasa kwa misingi ya soko. Tusitengeneze tu mpango kwamba tulime mazao haya zaidi, tulime kitu hiki au kile zaidi, hebu tuangalie soko lina uhitaji gani. Kama tunasema tuna uhitaji mkubwa wa mafuta ya alizeti, huko ndiko sasa tutengeneze mpango namna gani tunawashawishi wakulima ili waweze kulima alizeti na namna gani tunatengeneza sheria ambayo itazuia uingizaji wa mafuta ya alizeti kwenye nchi yetu ili soko letu la ndani lenyewe lianze kuwa ni soko kabla hatujategemea soko la nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu, lazima …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nianze na suala la utafutaji wa masoko ya bidhaa za kilimo.

Mheshiiwa Spika, ushauri Serikali iangalie mahitaji ya ndani ya bidhaa au mazao ya kilimo, kisha ifanye zoning ya kuhakikisha hitaji hilo litashughulikiwa na wakulima wa kanda fulani. Mfano tunahitaji mafuta ya kupikia nchini, hivyo ianishwe mikoa ambayo itatakiwa kuchangia market share hiyo. Hii itasaidia Serikali, kuelekeza nguvu kubwa za uwekezaji hasa katika utafiti, mbegu bora, upatikanaji wa masoko, kuweka miundombinu bora, pia itavutia wawekezaji.

Pili, miji yetu pia ni masoko ya bidhaa za kilimo kama mbogamboga, iangaliwe miji ambayo mito inapita katikati yake, halafu ifanyiwe mkakati wa kilimo bora cha mbogamboga na ufugaji wa samaki wa kizimba, bila kuathiri mazingira. Mfano Mji wa Iringa unapitiwa na Mto Ruaha, Njombe, Mto Ruhuji na kadhalika.

Tatu, fedha za wafadhili katika kilimo ziwafikie walengwa ikiwa ni pamoja na za Serikali zilizowekezwa kwenye mabenki ya Kilimo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi pia nishukuru kwa ajili ya juhudi kubwa za Wizara ya Afya na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anaendelea kuimarisha afya katika Taifa letu. Nawashukuru kwa ajili ya Kituo cha Afya Mkimbizi ambapo mmetupatia Shilingi milioni 250 na baadaye mmeongeza tena Shilingi milioni 250 nawashukuru sana, kwa ajili ya Wodi zinazojengwa katika Hospitali ya Frelimo ya Wilaya pale mawili na ICU pamoja na Mochuari. Nawashukuru pia kwa utanuzi unaoendelea wa Hospitali yetu ya Mkoa wa Iringa ingawa tuna changamoto kubwa ya upungufu wa watumishi, maana tunahitaji kuwa na watumishi karibu 466 na tuna watumishi 266 tu na nyinyi mmeipangia ile kwa ajili ya huduma ichangie zaidi ya Shilingi Bilioni 5.8 kwa hiyo tunaomba tuongezewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba leo niongelee hoja ya afya ya akili. Mheshimiwa Waziri nimesoma katika mambo yako sijaona sana unaongelea suala la afya ya akili, lakini afya ya akili ni kitu cha muhimu sana na ni lazima kama nchi tuhakikishe kwamba tunakichukulia uzito mkubwa na kukiwekea mipango. Kwa sababu, suala la afya ya akili tunaposema mtu awe na afya ya akili maana yake kwanza awe na uwezo wa kujitambua. Mtu anaonesha ana uwezo wa kutatua changamoto zake, mtu anaweza kufanya kazi na kuzalisha lakini mtu huyo anaweza akatoa mchango kwenye jamii yake. Sasa ukitaka kujua mpo kiwango gani cha afya ya akili kama wananchi lazima mjielekeze kuangalia hoja hizo. Kwanza kabisa tukienda namna gani labda kama Watanzania tunachangia ukiona mara nyingi raia wanajiuliza, Serikali inatufanyia nini na sio wao wanataka kusema sisi tunaifanyia nini Serikali ujue kuna tatizo kubwa kwenye afya yao ya akili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wote wenye afya za akili wanajiuliza mimi nitaifanyia nini Tanzania na sio Tanzania itanifanyia nini. Sasa sisi mara nyingi tunatumia Technic ya walevi au ya watu wanaopenda kunywa mara nyingi wako baadhi yao, wakiwa na tatizo anaahirisha tatizo kwa kulewa halafu kesho anajua akiamka mambo yatakuwa safi. Lakini kiuhalisia haiwi hivyo kwa sababu akiamka kesho fedha ile, ambayo anatakiwa aanze kutatulia changamoto ameitumia yote imekwisha. Suala hili lipo kwetu inapotokea changamoto mara nyingi tunakimbilia kutaka Serikali ifanye jambo bila kuangalia sisi wenyewe tunakwendaje kutatua lile jambo. Uwezo wetu wa kutatua changamoto kama wananchi/viongozi inaonekana umeshinda na hiyo ndio ina- comprise afya ya akili mna afya ya aina gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi juzi ikishuka bei ya mazao tunataka Serikali iweke ruzuku ikishuka bei ya mbolea tunataka Serikali iweke ruzuku imepanda bei ya mafuta tunataka Serikali iweke ruzuku. Sasa mimi najiuliza ni kwa nini hatufikirii kutatua changamoto na siku nyingine kutumia akili walizotumia wazee wetu, yamkini akili zao zilikuwa zina afya wakasema tunapita kwenye kipindi cha vita ni wakati wa kujifunga mikanda tuhakikishe tunapambana ili tujenge uchumi. Mimi leo najiuliza ile Shilingi Bilioni 100 tunayoiweka huku haijatoka kwenye TARURA kweli hatutaanza kutembea kwenye barabara zina makorongo, hatutaanza kukosa dawa? Sasa Mheshimiwa Waziri wa Afya tuangalie sana kwenye suala la afya ya akili, unatusaidia vipi tuweze kutatua changamoto zetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kujitambua ni ukweli usiopingika Taifa lolote linalotegemea kuendelea kuwa na nguvu, linafanya uwekezaji mkubwa kwa vijana wake na tunaposema vijana hapa ni miaka 15 mpaka 35. Sasa tuangalie kama Taifa tunawekezaje kwa vijana wetu unapofika mahali unaona vijana wa miaka 35 hawapewi priority wakati nchi nyingine sasa hivi zinahama zinaelekea hata kumpa kijana mwenye miaka 27 kuwa Rais wa nchi. Lakini sisi kwenye nafasi tu za Umeneja kwenye nafasi tu za Uenyekiti wa Bodi, tunajaa wazee na tunakaa sisi tu wakina bibi hili Taifa ni Taifa ambalo litafika mwisho. Kwa sababu, kama unaendelea kuwekeza kwa wazee unaendelea kila siku kuhuisha mikataba watu wamestaafu unakazi ya kuhuisha mikataba wazee waendelee wazee waendelee, maana yake ni kwamba vijana wako utawatumia lini? Utawapa practice lini maana huo ndio udumavu wa akili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu udumavu wa akili ni kama unashindwa kuwa na adequate simulation ile Sy social simulation ukishindwa kuwa nayo ile ina maana unashindwa kuwandaa vijana wako wajipange. Kwa nini kwenye hizi nafasi kama Profesa ni bibi basi msaidizi wa Profesa awe kijana mdogo ili kumuandaa. Kwenye nafasi kubwa tunashika sawa wewe umeshika nafasi kubwa ni mtu aged kwa nini hufanyi succession plan ya kumuandaa kijana. Sasa Taifa letu litakuwa halina nguvu kama siku zote tutaendelea kufikiri kwamba wanaoweza kushika nafasi kubwa, ni watu wenye umri mkubwa na kusahau vijana na hilo ni tatizo la afya ya akili. Kutotambua kwamba wewe ni mzee utaondoka nchi unatakiwa umuachie kijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri afya ya akili tunaiangalia sehemu nyingine sisi tunaweza tukaleta hoja kutoka huku chini lakini wenzetu mkikaa huko Wizarani mnatuona sisi kama... sisi tuko juu ndio wenyewe. Unaona sisi tuliwaambia ile Hospitali ya Mkoa wa Iringa mmeng’ang’ania kuitanua pale kwenye car seater pamejaa hata hapatanuliki mmebanwa na Magereza mmebanwa na Mahakama, pelekeni kwenye heka 35 kule mkaitanue vizuri nyinyi wenzetu mmekataa mmetuona sisi hatuna afya ya akili lakini kimsingi nyinyi ndio hamna afya ya akili. Kwa sababu, wewe unaweza kubadilisha Magereza iwe ICU kwa kuwaondoa Magereza pale? Nyinyi ndio hamna afya kwa hiyo sisi tunaomba muangalie. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Ummy hilo lisikupe taabu unafanya kazi vizuri mimi ninachoomba niletee Hospitali ya Wilaya ya Iringa, hujaiingiza hapa na uliniahidi kwamba basi tutakujengea Hospitali ya Wilaya lakini kwenye bajeti haipo mama yangu. Naomba kwa sababu sisi ile hospitali hatutibu watu wa Iringa tu na Majimbo yote yanayotuzunguka wanakuja pale, Isimani wanakuja, Kilolo wanakuja, kule kwa Kiswaga wanakuja, Kalenga na Mafinga wanakuja pale katikati tunaomba mtujengee hiyo hospitali yetu ya wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapoongelea afya ya akili angalia hali halisi ya performance ya Watanzania wetu. Leo hii unaweza kumuona mama amebeba begi zuri ukafikiri labda ndani ya begi mule sijui kuna nini lakini ukiangalia kuna maji ambayo amepewa sijui kwa Nabii gani yamletee magari, yamletee nyumba, yamletee utajiri, ana tango ameombewa sijui la kuimarisha ndoa, ana chumvi sijui ya kumwaga avute wateja, ana vitu kibao yaani vitu vinavyoonesha watu hawana afya ya akili. Wanadanganywa kwa hiyo Mheshimiwa Waziri wa Afya hiki ni kitu cha msingi, tunaomba ukiweke kwenye bajeti yako utatusaidiaje Watanzania hawa wawe na afya wasidanganyike? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna namna hata Mungu mwenyewe anasema nitabariki kazi ya mikono yako sio kwa kutembea na maji yaliyochotwa Jordan au maji yamechotwa Mto Meru sasa hili ni tatizo la afya ya akili. Hebu tuangalie afya za akili zetu wanasema afya ya akili ni kujitambua. Leo hii tuna vijana wengi wanaogopa kuoa wanaogopa kuolewa ukimuuliza wewe kwa nini huolewi anasema nipo nipo kwanza umri unakwenda, wewe kwa nini huoi nipo nipo kwanza. (Makofi)

Kosa la afya ya akili. Akili yake hai-reason sawasawa. Umri umefika, bado hajitambui. Sasa hiki kitu ni cha muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii afya ya akili tusipoishughulikia, ina tabia ya kuleta umasikini kwenye nchi, kwa sababu uwezo wa watu kuzalisha unapungua kwa sababu hawafikirii. Umenielewa? Leo nimekuja nikasema hapa jamani, wanaume hawa wanapendwa wakiwa na kitu (fedha), lakini kuna mwanaume mmoja anaitwa Heche, amelalamika kwa nini nimesema wanaume, sio warembo? Hilo ni tatizo la afya ya akili. Mimi siamini kama kuna mwanaume hapa atataka kuitwa mrembo. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, afya za akili za watu haziko sawasawa, mtusaidie. Watu wanalalamika ndoa zinavunjika kwa sababu ya suala la afya ya akili. Tumepeleka mikopo akina mama wakope, leo anakopa FINCA, anaenda PRIDE, anaenda huku anaenda huku. Ndoa nyingi zinavunjika kwa kuwa watu wanakimbia kwa sababu ya mikopo. Hajui namna ya kuzalisha. Unaona! Kwa hiyo, anakosa afya ya akili nini? Ya akili! Kwa hiyo, inatuletea matatizo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Jesca dakika zako zimeisha, lakini nakuongezea dakika moja, malizia mchango wako. (Makofi/Kicheko)

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, naendelea. Kama tunafikiri kwamba umasikini wa nchi hii utaisha kwa sababu ya kutoza kodi, mama aliongea categorically, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hatutaki kodi zenye dhuluma. Tunataka kodi kwa haki. Kama kuna kiongozi, bosi amekaa kwenye Ofisi ya TRA, anajua kabisa huyu mfanyabiashara uwezo wa kulipa hii kodi hana, halafu yeye anambambika kodi na kumtoza kodi kubwa, ni afya ya akili hana. Yeye mwenyewe analipwa kwa hiyo biashara, halafu anachagiza kuiua hiyo biashara. Ina maana mtu huyo hana afya ya akili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapokwenda na nguvu kufunga biashara, badala ya kumwelimisha mtu kwamba hii biashara fanya hivi na hivi, au nipe mpango wako wa kulipa kodi; wewe kazi yako ni kufunga biashara na wakati umetumwa ukalate na kuongeza mapato ya Taifa hili, afya yako ya akili ina mgogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana na viongozi wetu, tupo kwenye idara na kwenye Serikali, bado tunaona kuna vitengo. Mimi niko Kamati ya Nishati, nashukuru sana. Sisi tuna Kitengo cha Geothermal. Geothermal ni umeme wa jotoardhi, wamejipanga vizuri kupitia Waziri wetu anawasimamia, yule mzee tumefika anatusomea taarifa kwamba mimi nastaafu, lakini nimemwandaa kijana huyu hapa, anakuja kuchukua hii nafasi. Zipo Wizara na wapo mabosi wengine wa Wizara hapa, bado wanafikiri kuendelea ku-renew mikataba kwa wazee na wamesha-renew mikataba mara sita, mara saba. Wakati una-renew mkataba mara tatu mara nne, tayari tuna workforce ambayo ni vijana wamesoma hatuwaandai, ni kutokuwa na afya ya akili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nami naomba Mheshimiwa Ummy unapokuja hapa, useme hiyo afya ya akili unaiwekaje tupone?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii leo tena.

Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa hotuba nzuri ambayo Waziri Mkuu ameisoma jana ambayo imesheheni matumaini makubwa, lakini hoja yangu leo itakuwa ni umuhimu wa binadamu kutoa fursa kwa binadamu mwingine kuishi.

Mheshimiwa Spika, upo ukatili unaendelea juu ya binadamu na sisi tusipokuwa makini specie yetu kama viumbe hai kama binadamu tunakwenda kupotea.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema jana namna ambavyo Serikali imetekeleza mambo yake kwa mwaka ulioisha na fedha nyingi tulizowekeza huko, zaidi ya trilioni nane kwa ajili ya kutengeneza miundombinu mbalimbali ya kuhakikisha kwamba, ustawi wa binadamu katika nchi yetu unaendelea kuwepo. Naamini kabisa fedha nyingi tunazowekeza kwenye miradi ya kimkakati nia na madhumuni yake sio kutusaidia sisi tunaoishi leo peke yetu, tuna nia ya kuwasaidia watoto wetu, tuna nia ya kuwasaidia wajukuu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumewekeza zaidi ya bilioni 762 kwenye reli ambayo tunategemea itaishi zaidi ya miaka 100 ijayo na yamkini sisi katika miaka 100 ijayo sisi hatutakuwepo. Tumewekeza katika bwawa la umeme zaidi ya bilioni 800, Bwawa la Mwalimu Nyerere, hatutakuwepo. Tunawekeza katika miundombinu ya viwanja vya ndege zaidi ya bilioni 77 na Iringa tumepata bilioni 41 kwa ajili ya kujenga Kiwanja cha Nduli, kimefika asilimia 42 lakini tunajua tuliambiwa mpaka Septemba kitakuwa kimekamilika, tunajua zitaletwa fedha, lakini nia na madhumuni ni kwamba, tusaidie watoto wetu na wajukuu zetu na vizazi vijavyo, kama Watanzania na Waafrika.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza mipango ya maliasili za Taifa letu, jinsi tunavyotaka kuendelea kulinda maliasili zetu sio kwa ajili yetu sisi tu, kwa ajili ya watoto wetu na uzao ujao. Mama alivyojitolea kwa ajili ya kufanya ile movie ya Royal Tour, nia na madhumuni sio ataiona yeye peke yake na Awamu yake ya Sita, nia na madhumuni wajukuu wetu pia waje waione.

Mheshimiwa Spika, yapo mambo yanayoendelea katika jamii yetu. Tusipokuwa makini na tukienda kwa ku-copy na ku-paste kwa sababu, watu fulani wamesema au mataifa fulani yamesema, sisi tusipoamua kutumia akili zetu na kwamba, tumepewa fursa na Mungu na sisi kama Watanzania kuamua mambo yetu, upo wakati na sisi kama Watanzania tutoe fursa mataifa mengine yaje yajifunze kutoka kwetu namna ambavyo tunalea watoto wetu, namna ambavyo tunakuza watoto wetu.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Waafrika hatukufundishwa kujifunza tu kwa watu wengine. Afterall Mungu aliumba mtu mke na mume hakuangalia color ilikuwa ni color gani, kwa hiyo, na sisi watu wengine, mataifa mengine wanatakiwa waje wajifunze namna ambavyo Afrika inatunza watoto wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa katikati ukatili kwa watoto wetu umezidi mno. Tunashangaa, hatuelewi imetokea wapi? Imekuwaje? Waziri Mkuu ameeleza hali ya usalama wa nchi yetu na utulivu iko vizuri, mipaka yetu iko vizuri na ni kweli, wote tunashuhudia tuko vizuri, lakini kumbe ndani ya nchi kwenye uzao wetu tayari hatuko salama. Watoto wetu wamefanyiwa vitu vya hovyo mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo kumbe humu ndani tuna taasisi, tena Mheshimiwa Waziri Mkuu katika ku-wind up hotuba yake ameeleza mambo muhimu ambayo anataka yafuatwe. Moja katika yale sita, ameeleza jambo la tatu anasema, viongozi wetu wa Serikali, dini, mil ana vyama vya siasa wakemee kwa nguvu zote ushiriki wa sehemu yoyote ya jamii katika matendo yasiyoendana na mila, tamaduni na desturi za Watanzania. Hii ni pamoja na wazazi na walezi wote kushiriki kikamilifu katika makuzi na malezi bora ya watoto yatakayosaidia kuwaepusha na vitendo viovu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, it is a high time suala hili linalohusiana na ukatili kwa watoto wetu, ulawiti kwa watoto wetu, ubakaji kwa watoto wetu, masuala ya ndoa za jinsia moja yasifumbiwe macho. Tuyaongelee Makanisani, tuyaongelee Misikitini, tunaanza hapa Bungeni, tuyaongelee Serikalini, tuyaongelee kwenye familia zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutapotea. Hizi reli zitakuja kupandwa na popo kama ilivyokuwa Sodoma na Gomora. Huu umeme hautakuwa na maana. Haya majengo makubwa tunayojenga hayatakuwa na maana. Barabara ile wanayotujengea Iringa kwenda Ruaha National Park nani atapanda nani ataangalia wale tembo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema lazima binadamu mmoja atoe fursa kwa binadamu mwingine. Kama babu yangu mimi asingetoa fursa kwa baba yangu mimi leo ningekuwa wapi? Angemua babu yangu mimi aolewe na babu mwingine wa Kijiji kile ingekuwaje? Mimi leo ningekuwa wapi? Kama mama yangu angeona ndoa zina shida akaamua kuolewa na mwanamke mwingine, mimi leo ningekuwa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima vijana wetu waambiwe ukweli. Sisi tunawapenda, tunawaheshimu ndio maana tunawekeza, ndio maana mama hakawii anazunguka huko na huko kwa sababu ya kuhakikisha kwamba, tunalinda Watanzania na uzao wao. Sasa leo tukikaa kimya kwa sababu, ni human right, ni human right ipi wakati sisi hatutoi fursa? Sisi tulipewa right ya kuishi na moja among the human rights ni haki ya mtu kuishi na wewe unatakiwa kutoa fursa kwa mtu mwingine aishi, you don’t give the right halafu unataka upewe right, haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende kwenye shule zetu na si suala tu la Serikali kusema kwamba, sasa Serikali ije hapa maendeleo ya jamii watwambie hiyo jamii wanayoitunza ni ipi? Hii mipango tunayoitenga ya nini? Haya mabilioni ya fedha tunayaweka ya nini kama hayataangalia uzao wa tumbo letu? Kama hatutaangalia watoto wetu wanaishi vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo watoto wako kwenye vulgar environment, hawaelewi waende wapi. Wakija majumbani tafiti za UN zinaonesha kwamba, 66% ya watoto wanafanyiwa ukatili majumbani kwa wazazi wao, 44% inayobaki ni shuleni na sehemu nyingine. Wanakwenda shuleni tena wale guardians ambao tumewakabidhi watoto nao tena wanawalawiti watoto, wanawafanyia ubakaji watoto. Tanzania where is this country heading to? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi we need to be a role modal in this world. Other people should come also and learn from Tanzania kwamba na sisi tumeweza kuwa-groom watoto wetu, sio lazima tuige kila kitu from them. Hata wao wenyewe wame-confuse. Nimemsikia Biden mwenyewe anasema, anashangaa anasema my mum alisema tu it is sinful, halafu akasema it is cruelty kwa binadamu, ni ukatili kwa binadamu. Wenyewe hawaelewi, yaani they don’t know what to say. They find somewhere to read, wanataka mahali wakajifunze. Tanzania we are ready, tulikuwa tuna-raise vipi watoto wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Japani wanahangaika kwamba, uzao wao unakwisha kwa sababu, mwanamke ana uwezo wa kuzaa mtoto 1.3 kwa sisi tuliosoma hesabu maana yake kati ya wanawake wanne anayezaa watoto wawili ni mmoja tu. Wengine wanazaa mmoja wengine labda hawazai. Watu wanaona population yao inashuka, they are fighting, Waziri Mkuu yule ana-fight namna gani ainue population yake. Sasa kama it is a human right wao kuoana wanawake kwa wanawake na wanaume kwa wanaume kwa nini wanawa- force watoto wetu waingie kwenye hizo kwa kuwalazimisha kufanya vitu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wao nao wa-grow wafike waamue wenyewe. Nashindwa kuelewa NGO ndani ya nchi hii. Nimerudi Iringa nimekutana na hiyo, vijana wananiambia kuna mahali mmetupeleka tukafundishwe tukopeshwe, lakini madam mbona kama vile wanatufundisha mambo fulani? In this country! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumewaruhusu, halafu hiyohiyo Wizara ya Maendeleo ya jamii, hiyo hiyo ndio inasajili NGO, hiyo hiyo ndio inatakiwa kulinda jamii, hiyo hiyo ndio inatuletea watu wanagawa vilainishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, look here, we are privileged to be leaders in this country. Ni neema, it is a grace. Tusije tukajiona kwamba, sisi ni wa maana sana kuliko watu wengine, we are graced na tusipotumia neema hii vizuri, leo tukikaa kimya Mungu atainua mawe yatasema, ila sisi na uzao wetu utapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudia tena, binadamu atoe fursa ya binadamu mwingine kuishi. We love them, they are our kids. Ni watoto wetu, tunawapenda, hata hawa walioingia kwenye mifumo hiyo ya ndoa za jinsia moja au ushoga hatuwachukii ni watoto wetu, mtoto wako hata akiwa kibaka utamkataa?

Mheshimiwa Spika, tutafute mbinu za kuwasaidia wale watoto wetu. Tuone namna gani tutakaa, kama we think kwamba, dunia ime-advance scientifically let that science prove kwamba, inaweza ku-solve problems kama hizi. Science ituhakikishie kama inaweza kumsaidia kijana wetu wa kiume aliye-engage huko, amepoteza kabisa viungo vyake, nguvu zake hazi-function, itusaidie. Hatujamaliza bado kupambana na matatizo ya uzazi wa wanawake, leo tuanze kupambana na kubadilisha matumbo ya wanaume yawe ya akinamama, inawezekanaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya tu ambayo ni original tumepewa bure tumeshindwa kuyashughulikia…

SPIKA: Mheshimiwa Jesca Msambatavangu muda wako umeisha. Dakika moja, malizia.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba Waheshimiwa Wabunge tusimame kwa pamoja. Kwa agizo hili twende kwa pamoja, ukisimama hapa wekaweka kidogo mbwembwe, haiwezekani, Ubunge wetu hauna maana kama watoto wetu hawatakuwepo baada ya miaka 10. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuko tayari kuacha Tanzania iwe ni nchi kama ilivyo Sodoma na Gomora wanazaliana popo. We are not ready, we are here ku-make sure Watanzania wanaendelea kuwepo katika ulimwengu huu mpaka ukamilifu wa dahari, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote na mimi nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mchango wake mkubwa kwenye sekta ya afya, akisaidiwa na Waziri wetu Ummy, Waziri makini kabisa na Naibu Waziri Kaka yangu Mollel. Tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na Kamati, nawashukuru sana kwa kuja Iringa na kuona changamoto zilizopo katika Hospitali yetu ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa. Tunawashukuru sana kwa ajili ya Digital X-Ray Scan na ukarabati wa lile jengo la Radiology ambalo mmetumia zaidi shilingi bilioni moja na milioni mia saba na tisini na moja, tunawashukuru sana pia kwa ukarabati wa ICU shilingi milioni 150, tunawashukuru sana. Tunawashukuru pia kwa ajili ya fedha nyingi mlizozileta kwenye hospitali yetu ya Wilaya ya Manispaa ya Iringa ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni moja na milioni milioni mia mbili. Tunawashukuru kwa ajili ya fedha ya Kituo cha Afya Mkimbizi shilingi milioni 500. Tunawashukuru kwa ajili ya fedha katika Kituo cha Afya Ipogoro shilingi milioni 357. Tunawashukuru kwa ajili ya fedha mlizoleta kwenye zahanati zetu, Zahanati ya Mkwawa shilingi milioni 50, Zahanati ya Isakalilo pale shilingi milioni 150, Zahanati ya Nduli shilingi milioni 50, Zahanati ya Ugele shilingi milioni 50. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya changamoto zilizotokea tunaomba muendelee kutuongezea watumishi katika Hospitali yetu ya Referral ya Mkoa wa Iringa na pamoja na kwamba mmeshatupatia watumishi wengine karibu 26 lakini bado tuna upungufu. Mmetupatia watumishi 46 kwenye Hospitali yetu ya Wilaya bado tuna upungufu na katika vituo vyetu vya afya kwa mfano Mkimbizi mmetupatia watumishi Saba. Tunawashukuru sana na kwenye zahanati watatu, watatu tunawashukuru tunaomba muongeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, Manispaa ya Iringa kwa geographical location yake inahudumia siyo Manispaa ya Iringa tu. Tunahudumia Jimbo la Kalenga, tunahudumia Isimani, tunahudumia Kilolo. Kwa sababu watu hawawezi kupita pale Mjini wakaenda kutibiwa Kilolo wakati pale kwenyewe kuna Hospitali. Hawawezi kutoka Kalenga wakapita mjini wakaenda kutibiwa Igodivaa wakati pale kuna hospitali. Hawawezi kutoka Ifunda wakaja kutibiwa huko Igodivaa. Kwa hiyo location yetu tunaomba sana mtusaidie. Mtuongezee kituo cha afya Kitilu, mtuongezee kituo cha afya Igumbilo kwa sababu huko ndiko kunakopokea watu kutoka kwenye Majimbo mengine na sisi tupo tayari kwa sababu kwa mfano Igumbilo pekeyake zahanati inahudumia zaidi ya watu 600. Sasa unaweza kuona mzigo unavyokuwa mkubwa. Kwa hiyo tunaomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ufinyu wa eneo katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa ni changamoto ambayo kamati imesema. Mimi niwaombe rejeeni mapendekezo yetu na RCC ya Iringa, kwamba Hospitali ya Wilaya ile ina eneo kubwa sana na wala pale siyo mbali hazifiki hata kilometa Sita. Mnaweza mkaamua structure zenu nyingine mkaziweka pale na mkatenga kama mkoa ili tuendelee kupata huduma za referral kwenye hospitali yetu ya Mkoa kuliko kufikiria kuihamisha pale Wizara ya Mambo ya Ndani ianweza ikawa shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunaomba wataalamu wa mifupa. Mnaona geographical location ya Iringa, ipo kati kati pale, barabara kubwa zote zinapita pale, ajali ni nyingi. Kwa hiyo, wote wanategemea kuja pale kwa ukaribu wake. Tunaomba sana wataalam wa mifupa, masikio tupate ili watu wakipata ajali kuliko kuanza kuwakimbiza Benjamin kuwapeleka Muhimbili, na distance ni ndefu, basi pale tupate wataalam wa mifupa ili waweze kutusaidia lakini tunawashukuru kwa ajili ya wataalam mliotuletewa wanne kwa ajili ya viungo bandia kwa ajili ya wagonjwa wa ajali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwashukuru sana pia kwa kuniteua kuwa Balozi wa Afya ya Akili Tanzania. Nakushukuru sana Waziri wa Afya na ninaona jambo hili linaongelewa kwa mapana yake. Sasa katika huo ubalozi naomba basi wale Isanga wanatibu tibasheria, kwa ajili ya wale wenzetu wanaoonekana kule kwenye sheria walipelekwa kimakosa kumbe ni matatizo ya afya ya akili wanapelekwa pale kusaidiwa kutoka Magereza. Wapeni basi hiyo shilingi bilioni moja na milioni 600 walizoomba changamoto ya kibajeti ili waweze kuwahudumia wenzetu wenye matatizo ya afya ya akili kutoka kwenye vyombo vya sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru pia kwa ajili ya Mirembe kuifanya kuwa Taasisi ya Afya ya Akili Nchini. Ilingane lingane basi sasa na taasisi ya afya. Tumesherehekea mwaka jana miaka 100 pale lakini bado hapaeleweki. Ilingane na taasisi ya afya ya akili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri kama Balozi nisipoongelea masuala ya afya ya akili nitakuwa sijaitendea haki nafsi yangu mimi mwenyewe. Masuala ya matatizo ya afya ya akili ni makubwa. Ninakushukuru umeweka katika vipaumbele vyako Namba Sita kuimarisha huduma za afya ya akili, huduma za utangamano na tiba shufaa. Tunakushukuru sana kwamba umeiingiza lakini ipe uzito unaowezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ummy, matatizo ya afya ya akili yanakuletea cost kubwa sana kwenye vifaatiba na matibabu. Kama WHO wanasema afya ya akili ni kutojitambua, ni kushindwa kupambana na changamoto, ni kushindwa kutoa msaada kwenye jamii, ni kushindwa kufanya kazi kuzalisha kwa faida, hiyo ilitakiwa ipewe kipaumbele cha kwanza. Tukiwapa watu wetu wakawa na uelewa mzuri kwenye akili zao. Kwanza mimi nataka ile pre copying kwanza. Kabla hujafikia kutupa dawa za afya ya akili, tujifunze kwanza masuala ya mambo yanayosababisha tukafikia kule kwenye kutumia dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hiii tuifanyaje? Tufanye kampeni maalum. Marekani tangu miaka ya 50 wana mwezi wa kampeni maalum kwa ajili ya masuala ya afya ya akili na wao wanaifanya Mei. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasi tuchague mwezi maalum ambao tutaongelea masuala ya afya ya akili, tutawaambia watu wafanye meditation, tutawaambia watu mwezi huu nendeni mkafanyiwe massage, tutawaambia watu mwezi huu walie wasiolia, tutawaambia watu mwezi huu ni wa kusema matatizo yenu ili watu waseme, watu walie, watu wapate nafasi ya kwenda kufanya massage, watu wapate nafasi ya kwenda kutembelea misitu, waende national parks, waka-relax akili zao. Wakirudi wawe salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri haya matatizo ya afya ya akili ndiyo yanakufanya wewe unakuwa na wogonjwa wengi wasio na magonjwa ya kuambukiza hospitali. Unatumia fedha nyingi, kumbe watu wanatakiwa kufanyiwa tu mazoezi, watu wakishachangamana humu kwenye ndoa wakashindana wakidundana ngumi wanakuja kushonwa kwako wewe. Wanapiga x-ray mzigo unaongezeka kwako. Watu wakishindwa kufanya maamuzi sahihi wanawasababishia wengine presha. Ndiyo unapata taabu kubwa wengine veins zina-fail ndiyo tunapata taabu kubwa ya kununua ma-CT Scan kumbe mambo mengine yangetibika. Hapa umetuambia umetibu watu milioni 35.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naongea na daktari mmoja akasema katika watu 10 wanaoenda hospitali, wagonjwa ni Watatu, Saba wote hawa wameenda kwa sababu tu ya afya ya akili. Mtu tu mke wake kaamua kumletea tatizo kwenye nyumba, mume amefyatuka presha iko juu, anahitaji CT scan anahitaji vitu kama hivyo. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunatakiwa sisi tuone kwamba kampeni ya afya ya akili ndiyo kitu cha mwanzo kuliko vitu vingine. Ukija mimi ukaniahidi hapa leo kama Jesca Mbunge, ukaniahidi kwamba chinga wa Iringa tunakwenda kuwaletea shilingi milioni 700 watengenezewe structure zao, halafu usipoleta zile fedha mimi umenifanya niwe chizi, na wale machinga wangu wote wamekuwa machizi, hivi hatueleweki afya zetu zimeyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii kampeni ianze kwenye Wizara za wenzio wasiwe motor behind kusababisha afya za akili waambie mnanivurugia watu afya zao. Ahadi ziwe zinatekelezeka, mipango itekelezeke ili watu wawe na afya nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, afya ya akili inakwenda kwenye masuala ya imani. Mtu akili ikishashindwa kufika mahali ikaamua jinsi ya kutatua tatizo lake anajipeleka sasa kwenye imani potofu, ndiyo kule wanafikia sasa mtu anaambiwa ukienda ukambaka mzee, ukambaka mtoto, ukambaka dada yako, ukambaka mama yako unapata utajiri. Sasa mwisho wa siku wakibakwa wanakuja kwako Waziri wangu Ummy wanahitaji dawa, wanahitaji huduma za afya, tunaongeza mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala hili liweke mwanzo. Kampeni ifanyike kubwa ili watu wetu waelewe kwanza. Katika vitabu vya Mwenyezi Mungu vinasema watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Kitu cha kwanza kinachomuangamiza binadamu ni kiuchumi, kisiasa, kinachomuangamiza kwenye jamii ni kukosa maarifa. Kama mtu hana understanding ya kwamba kulia ni deal, kulia kutaniponya, kwenda National Parks kutembea Selous kutaniponya, anafikiri ni anasa peke yake inatupa shida, mtu aelewe kwamba kwenda National Park siyo anasa unakwenda kufanya healing. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenda na watoto wako kuogelea wakati mwingine kutembea na watoto wako porini wakasikia harufu tofuti tofauti, sauti za ndege badala ya sauti za magari peke yake, ile nayo ni healing ya kutosha. Wewe kuendelea kusema mimi leo namtoa outing mke wako na ukasema leo simtoi mchepuko outing, namtoa mke wangu outing umemfanyia healing akirudi hatakusababishia matatizo ya afya ya akili, lakini watu wanadhani ni anasa.!

Sasa hivi Mabalozi tuko well empowered, tunaweza kufundisha watu Mheshimiwa Ummy hapa sasa bajeti ya Balozi iwepo maana yake sasa hata bajeti ya Balozi haipo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mambo haya Mheshimiwa Ummy nimekuwa nayafanya mwenyewe kivyangu, hayawezi kwenda kwenye upana huo. Tengeneza timu sisi twende tukawaambie watu. Tukaongee na vijana wetu, tuwaeleze. Hii tabia ya mtu kujiona eti mimi mwanamke lakini I am feeling, I am a man yaani yeye ni mwanamke anajiona ni mwanaume, no! hatuangalii jinsia kwa kujihisi, tunaangalia kwa structure uliyonayo kwa physical appearance yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo tunaongea hapa ushoga, tunaongea sijui usagaji kumbe watu wangekuwa vizuri tu, hana sababu ya kujiona mwanamke mwanaume, mwanaume mwanamke kwa sababu tayari akili yake inge- sense tu kwa kiungo nilichonacho mimi ni mwanamme sina sababu ya kujiona mwanamke. Kwa kiungo nilichonacho mimi ni mwanamke, sina sababu ya kujifanya mwanaume.

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Balozi.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia suala lililopo mbele yetu, Azimio la Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Bara la Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba leo niongee mambo mawili makubwa ambayo huwa tunayapata baada ya kupitisha maazimio katika Bunge lako Tukufu. Awali ya yote, nipongeze mtazamo wa Wizara kwa ujumla kwa sababu dunia inapokwenda sasa hivi, sisi hatuwezi kukaa kama kisiwa. Dunia imeshakuwa globalized, mambo yanafanyika kwa pamoja. Kwa hiyo, nawapongeza sana kwamba inawezekana hata kuridhia Azimio hili tumechelewa. Kwa kuwa sasa tumeamua kuridhia, nitakuwa na ushauri wangu katika mambo mawili kwa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni timing au kwenda na muda. Jambo la pili ni mindset, jinsi ya kuandaa akili za Watanzania ili kwenda sawa na mipango ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na timing, kila kitu lazima kiwe na muda maalum na ili ufikie malengo unayopanga, lazima ujipangie muda. Kamati imeeleza vizuri sana na imetoa ushauri mzuri sana kwamba tunakwenda kuridhia itifaki hii, cha msingi, ni lazima Serikali iangalie sera zetu, kanuni zetu na sheria zetu ziendane na wakati. Maana tunaweza tukaridhia hili, bado sheria zetu zikachelewa kurekebishwa, na kanuni zetu zikachelewa, bado na sera zetu zikawa ni zile zile, haitakuwa na maana ya sisi kuridhia haya. Kwa hiyo, tunaomba haya mambo tunapoyapitisha, yaendane na kasi na muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu Iringa kuna usemi tunasema hivi: “Ng’ombe anayewahi kufika mtoni, ndiye anayekunywa maji masafi.” Kwenye biashara kuna watu wanaoitwa innovators. Wale watu ambao ni innovators mara nyingi hawafilisiki na ndio ambao huwa wanaendelea, wanarithisha utajiri kizazi na kizazi. Wale ambao wanajifunza kwa kuangalia matokeo, mara nyingi ndio wale ambao wanafilisika kila wakati. Mtu ambaye anabuni kitu akakianzisha mwenyewe, mwingine anasubiri mwenzie abuni, aangalie kama atanufaika, yule ndiye ambaye sasa anakuja kufilisikafilisika na biashara zake haziendi vizuri; lakini mtu yeyote anayeangalia mapema akawahi ile fursa mapema, ndiye anayeweza kufaidi na kunufaika na hiyo fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaridhia Azimio hili kwa nia ya kwamba sasa tunaenda kuboresha utalii wetu, tunaenda kutanua mipaka yetu ya kunufaika kibiashara kwenye nchi ambazo zinaridhia Azimio hili, lakini wenzetu watanufaika, watafaidi kwenye nchi yetu, na sisi watu wetu wakawa bado wana-lag behind au bado hatujawaandaa katika ile attitude, ndiyo unakuja sasa kwenye aspect namba mbili ya mindset. Ni namna gani tunawaandaa watanzania kwenye haya maazimio mazuri ambayo Bunge linayapitisha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, akili za Watanzania huwa zinashibishwa vipi maarifa, wakaelewa nia dhabiti ya Serikali inayokuwemo ndani ya haya maazimio? Kama tunapitisha hapa maazimio na Watanzania akili zao hazijaelewa vizuri, bado wanaona tunapoteza muda, lakini huwa yanageuka yanakuwa fimbo. Tunapitisha kwa nia njema kwa kuangalia ustawi wa Watanzania, kwa kuangalia kukua kwa uchumi kwa Watanzania, kwa kuangalia tunavyoongeza fursa za ajira, kwa kuangalia tunavyobadilisha maendeleo ya Watanzania, lakini kwa kuwa mindset zao ambazo zinakuja kuleta attitudes zao hazikusetiwa vizuri, yanatugeuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepitisha maazimio, lakini watu hawajui. Mheshimiwa Waziri lazima tukubali kwamba katika bajeti zetu tunatumia gharama kuwaelimisha watu. Mwalimu alishasema, kama wewe unaona kwamba elimu ni gharama, basi jaribu upumbavu au jaribu ujinga. Kama tunafikiri kwamba tutapitisha maazimio halafu Watanzania hawayaelewi yakaenda yalivyo, hebu tujaribu sasa kuyapitisha maazimio, watu hawayaelewi, halafu uone yakifika kwenye jamii jinsi yanavyoturudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatakiwa kuwekeza nguvu kubwa kwenye kuhakikisha kwamba watanzania wanaelewa nini hasa nia nzuri na dhabiti ya Serikali kwa kuwapa elimu waelewe. Usipom-set mtu vizuri kwenye akili aka-download uongo akauweka kwenye moyo wake, kuja kuutoa huo uongo aliouweka moyoni ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali, kwenye maazimio kama haya yasiishie tu hapa, lazima kuwe na program maalum ya kuhakikisha Watanzania wanaelimishwa, wanawekwa sawasawa, waelewe nia thabiti ya Serikali yao, kwamba nia ya Azimio hili ni kutanua mipaka yetu hata ya ajira. Hatuwezi tukakaa humu ndani ya Tanzania…

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: … na Watanzania milioni 61 tukafikiri kwamba tunaweza kuajiri wote humu tukapata fursa, wakati kuna fursa ya ajira sehemu ya watu milioni 360…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jesca, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Engineer Mwanaisha Ulenge.

TAARIFA

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Napenda kumpa taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Msambatavangu kuwa katika hilo analolisema, ni jambo jema sana na Umoja wa Mataifa tayari imeshaweka Azimio la kwamba sharing misinformation can seriously harm those around you. Nafikiri ni wakati sahihi sasa ili watu waweze kuelewa maazimio yanayotolewa na Serikali kwa usahihi, tuunge mkono jitihada za Umoja wa Mataifa katika kampeni hii ya watu kuto-share taarifa zisizokuwa sahihi bila kuwa na uhakika wa taarifa hizo, ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jesca, taarifa unaipokea?

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili, taarifa ya Engineer iliyoenda shule.

Mheshimwia Mwenyekiti, tunaambiwa kwamba taarifa ni nguvu. Azimio hili limeongelea, na sifa kubwa ya nchi yetu ni kuwa na amani na utulivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie amani na utulivu huwa inaanza kwanza kwenye choko choko za kupotosha taarifa. Tutachokonoa Mhimili wetu wa amani na kukorofishana humu ndani na tukapigana na tukaonekana hatuko sawa sawa baadaye tunakuja kuambizana kumbe kuna muongo mmoja alianzisha tu taarifa akaipeleka yeye isivyo wakati wenye taarifa sahihi hawakuzifikisha wakati sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe maazimio haya yamilikiwe na Serikali kama mnavyotumilikisha Wabunge na Watanzania wayamiliki haya ni mambo ya nchi yetu, wawe wanaelewa tuna desturi moja. Isiwe rahisi mtu anakuja tu kutuambia tumeuzwa, watu wengine pressure zinapanda mmeuzwa, mmeuzwa, mmeuzwa watu wanafikili. Mtu mwingine anaweza akatoka hapa na hili hili azimio akaenda kusema mmekodishwa, mmekodishwa SADC watu wakaona tumekodishwa au tumepangishwa. Kumbe nia siyo hiyo nia ni thabiti watu wapewe elimu tutumie fedha kutoa elimu kwa Watanzania wawe wanaelewa mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utali ni package, Watanzania waelewe utalini package, mtalii anataka kutoka Afrika Kusini mpaka Cairo atumie ile nini wanasema Cape to Cairo apite nchi zote ndani ya Afrika akafike Cairo atoke Kusini mpaka kule. Sasa sisi tukikaa tumejifungua hapa hatujaridhia azimio hili tumetanua utalii wetu kupitia royal tour watu watatoka Marekani watakuja Tanzania watataka kwenda Congo tayari kuna vifigisu figisu sisi hatujafungua mipaka na kushirikiana na wenzetu wa Congo utalii hautokua? mindset za Watanzania hapo wengine tayari ukishaambiwa tu nchi nyingine kama Congo unajua ni vita tu, ukumbuki kumbe na akina Awilo Longomba nao watatoka huko huko kama kuna vita tu hakuna mambo mengine ya starehe kwanini wanaweza kupata muda wakajifunza na muziki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii ni ku-unset mind zao wajue kwamba kuna fursa kwenye nchi zingine; lazima Watanzania wapate maarifa haya. Ndugu zangu tusipo wekeza kwenye mind set na altitude tunapitwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda nchi kama Nigeria wanakwambia moja ya sehemu ambapo wameajiri watu wengi ni kwenye utume ni missionary namna ambavyo wameshirikiana na Taasisi za kidini halafu wamezifundisha zile Taasisi za kidini wamezi-empower kwa kutengeneza kanuni na sera nzuri wamewaruhusu dini waende nje ya mipaka ya nchi yao. Kwa hiyo, wameweza kufungua huko mamisikiti, wameweza kufungua huko makanisa kwa watu wengine wamekwenda kuajiriwa hata nje ya Nigeria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunajipanga vipi kuhakikisha kwamba tunashirikiana na wenzetu, siyo tu sisi Watanzania, Taasisi za dini kuona kwamba tunawaita Viongozi wa dini tukawaambia kuna fursa hizi tunaomba mnaposimama mkitoa maelekezo yenu, mkitoa na nyaraka nyingine toeni na fursa hizi hapa ili Watanzania wajue kuna fursa sehemu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hayo hatutayafanya tutabaki kulaumiana na tutaonekana sisi tunaandika vizuri sana, tunamipango mingi sana, tunamaazimio mengi tunapitisha lakini hayana tija kwa Watanzania…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jesca ahsante sana, malizia sentesi ya mwisho.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri, narudia tena lazima tuhakikishe tunawekeza kwenye fahamu. Watu wetu wajue na wewe ndiyo Waziri wa Viwanda na Biashara, watu wetu wajue ni kitu gani hasa kiko ndani ya hili azimio?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niungane na wenzangu, lakini kabla nataka na mimi niweke msingi kama ambavyo makubaliano haya yanaweka msingi na msingi wangu nitauweka kutoka kwenye vitabu vya Mwenyezi Mungu, nita-refer Biblia.

Mheshimiwa Spika, Hosea 4:6 inasema; “Watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa, kwa kuwa wameyakataa maarifa.” Mathayo 22:29 inasema; “Yesu akajibu akawaambia mwapotea kwa kuwa hamyajui maandiko.” Yohana 8:32 inasema; “Tena mtaifahamu kweli na hiyo kweli itawaweka huru.” Methali 11:9 inasema; “Asiyemcha Mungu, humpoteza jirani yake kwa kinywa chake, bali wenye haki watapona kwa maarifa.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naanzia hapo, hofu zetu zote ni kutokuwa na maarifa na Serikali inachokifanya sasa hapa leo imetupa maarifa ya kutosha, tuondoe sasa ile dhana yetu tuliyokuwa nayo kwenye vichwa, tukubali kuingiza vitu vipya, ili tusiendelee kudanganywa na kuangamia. Mimi kwa kuwa somo la sheria na mimi pia nilipata kidogo ukakasi, lakini sikutaka kuangamia kwa kukosa maarifa. Nilijipa muda wa kusema nitafute maarifa. Kwenye huu mkataba kwanza kitu cha kwanza unachotakiwa kujua unakwenda kwanza malengo yake ni nini.

Mheshimiwa Spika, kwa sisi tusio wanasheria, watu wa biashara tunapoandika research huwa kuna general objectives na kuna specific objectives. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo la jumla la mkataba huu ni kati ya nchi na nchi na hawa nchi na nchi wanaingia makubaliano ya kushirikiana kwenye masuala ya biashara kwenye maeneo ya bandari, automatic bandari zinakuwa kwenye maziwa, kwenye bahari, kwenye mito, hiyo ni ya ujumla na hii utaipata kwenye ibara ya pili; malengo ya mkataba.

Mheshimiwa Spika, ukija Ibara ya nne ya mkataba ambayo inaeleza mawanda au upana ndiyo hiyo tulikuwa tunasema scope, hii imejaribu kuelezea mawanda ya huu mkataba lakini imekwenda specific kwamba hawa nchi wameshaingia makubaliano na wenzetu wale wanafikiri kwamba kampuni ambayo labda inaweza tukaanza nayo ni ya kwao ya uwekezaji kwenye bandari ambayo ni DP World.

Mheshimiwa Spika, wakai-bind kabisa kwa specific objective kwamba ninyi mkienda Tanzania mtaingia mkataba baada ya kuwa hatua zote zimefikiwa pamoja na Bunge kuridhia, mkataba wenu mtakwenda kuingia kwenye maeneo haya. Ndio hiyo appendix moja tuliyoisema imeeleza kwa undani, lakini kilichonifurahisha katika kujua malengo, siyo kwamba bandari zote au maziwa yote au Tanga sijui huko Mtwara wapi zimeingia, hapana. Kwenye hiyo hiyo article four namba mbili inasema; Tanzania will inform Dubai of any other opportunities relating to ports, freezones and logistics sectors in Tanzania to allow Dubai or Dubai entities to express interest and submit proposals for consideration in respect of such other opportunities.

Mheshimiwa Spika, kwamba sisi Tanzanaia ndiyo tutakuwa na mamlaka ya kuwaambia wale Dubai tuna fursa nyingine huku labda kuna Bandari ya Mtwara tunaomba kwa sababu hapa mmefanya vizuri, tunaomba basi na Mtwara mkafanye kitu kama hiki. Wao watakuwa na responsibility ya kutafuta mtaji na kwenda kuendeleza, kusiamia na kuhakikisha wanaboresha. Hivyo ndivyo mkataba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa wanasheria wakisoma wanatudanganya kwamba maziwa yote yamechukuliwa, bahari zote zimechukuliwa, mbona namba mbili hamuiangalii kwamba consideration ni sisi ndio tutakao-inform hawa kwamba tuna opportunities nyingine katika hizi water bodies za uwekezaji wa bandari, hapo mimi nikajiridhisha, nikaondoka na kuangamizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama mwanasiasa kuna hoja nyingine utaifikiria kwamba je, ardhi ya Watanzania inachukiliwa? Maana ardhi ikishachukuliwa Tanzania maana mimi watu wangu watakaa wapi? Wapiga kura wangu Iringa watakaa wapi au wataenda wapi? Nikaenda Ibara ya nane inaeleza ukurasa wa 18 haki ya ardhi, lakini hapa Ibara hii inaitaka Serikali ya Tanzania kuhakikisha hatua muhimu zinachukuliwa ili kuwezesha DP World kupata haki ya matumizi ya ardhi. Yes, lazima sisi kama Watanzania tuwa-guarantee wale matumizi ya ardhi yetu. Wanaleta mitambo, sawa, watawekeza pale. Sasa kama hatutawalinda kwa sheria zetu tukaendelea kuwa na urasimu, tukaendelea kuwa-disturb, unategemea wawekezaji wataendelea kuwepo?

Mheshimiwa Spika, sisi tumepewa jukumu la kuwalinda hawa wawekezaji na ni jukumu la msingi, sio kumiliki ardhi. Katika hii ukurasa wa tisa inaeleza tafsiri, hakuna mtu anakuja kumiliki na kuchukua ardhi ya Watanzania. Ukurasa wa tisa, Land Rights inavyoeleza interpretation inasema; “Land Rights shall mean all those rights (excluding rights of ownership of the land in Tanzania.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imeondoa hilo suala la umiliki wa ardhi, kwa hiyo wao watakuwepo kwenye matumizi ya ardhi. Sisi tunasoma hivi, ili tusiangamie hata kama sio wanasiasa. (Makofi)

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, manufaa kwa Watanzania...

SPIKA: Mheshimiwa Jesca Msambatavangu kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei.

TAARIFA

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nataka kusema kwamba huu mkataba na anavyozungumza vizuri sana Mheshimiwa wetu, jina lake gumu sana, Mheshimiwa Jesca, ni kwamba wanaangalia logistic ya from Dar es Salaam na kufikisha mzigo Burundi, Rwanda kote na Uganda. Kwa hiyo, lazima wafikirie kwamba ili iwe ni efficient lazima waweze kuboresha bandari za Ziwa Victoria, kama itakuwa hivyo na pia waweze kuweka maeneo ya bandari kavu sawasawa na kadhalika na pia kuwezesha hizi export… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Jesca Msambatavangu, unapokea Taarifa hiyo?

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nashukuru sana kwa Taarifa; fahari ya wazee ni mvi kichwani, hiyo ndio hekima ya mzee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwamba wewe huwezi kumpa mtu atoe makontena pale usimpe sehemu ya kuweka makontena. Huyu DP World ana bandari kavu Rwanda, usimpe access ya treni kwenda Rwanda kupeleka makontena yake; ana-supply na South Africa, sijui na wapi huko na Djibouti huko ana mikataba inaendelea, usimpe access kwamba atakwenda hadi huko kupeleka makontena, haiwezekani. Kwa hiyo, ndio maana kuna appendix II kwamba, badae tutakuja kuendelea kuongea sisi tutakapokubali tutamshirikisha yeye.

Mheshimiwa Spika, kama mwanasiasa manufaa hayo mengine ya ushirikishaji, tatizo kubwa tulilonalo saa hizi ni ajira. Mimi nikaangalia changamoto, hivi mimi watu wangu wa Iringa wanaosoma pale Chuo cha Bandari, Dar es Salaam watapata kazi au ndio zinakwisha au wanafukuzwa?

Mheshimiwa Spika, nikaangalia Ibara ya 13 - ushirikishwaji wa wazawa, ajira na majukumu kwa jamii. Tunahangaika hapa kutoa ajira, tunaleta wawekezaji ili tupate ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, anasema ibara hii, inaelekeza kuwa mikataba itakayosainiwa ya utekelezaji wa mradi lazima iainishe mpango wa ushirikishwaji wa wazawa katika utekelezaji wa mradi husika, unaona? Na maeneo yafuatayo yatapewa kipaumbele kwenye hii article. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo inasema kutoa kipaumbele kwa kampuni za ndani katika zabuni na ushauri pale ambapo makampuni hayo yatakidhi vigezo. Baadhi ya miradi inayokwenda kutekelezwa iwe imetolewa kwa kampuni za ndani na raia wa Tanzania; kutekeleza mpango wa mafunzo ya uendelezaji wa raia wa Tanzania; kusaidia kujenga uwezo wa vyuo/mafunzo katika tasnia ya usafiri majini na usafirishaji; na kuwezesha tafiti na uhamasishaji wa teknolojia kwa wazawa.

Mheshimiwa Spika, hii tayari msingi umewekwa wazawa wetu sisi…

SPIKA: Sekunde 30 malizia.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, wazawa watapata ajira, lakini na wale waliokuwepo wataboreshwa kwa kupewa mafunzo. Maana asije akasema nimeweka kitu cha kisasa hapa Mtanzania hawezi, tunataka ampe mafunzo aweze kuki-operate kile kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka nini?

SPIKA: Haya, ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, mimi naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Mpango huu wa mwaka 2022/2023. Pia nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wengine kuendelea kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anajali sana hali za wananchi wetu, hasa kwa kuangalia kuwekeza kwenye elimu, afya, maji na miundombinu ya barabara. Tunamshukuru sana na tunamwombea Mungu aendelee kumpa afya na hekima katika kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapomshukuru Mheshimiwa Rais naomba pia Mheshimiwa Waziri wa Fedha anapoandaa hii Mipango, kwa kuwa Mama sasa ameshafanya lile jukumu lingine ambalo lilikuwa ni madarasa na sehemu nyingine, kwenye afya na vituo vya afya, basi awe anatuletea pia na taarifa ya yale mengine tuliyoyapanga sisi wenyewe humu ndani, yanakwenda vipi? Zile chenji za fedha ambazo zingebaki au zilitakiwa zitumike, hazijatumika, zimeendaje? Tunaomba hilo tuwe tunaambiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri wa Fedha awe anatuambia pia, katika Mpango huu aliousoma na Kamati ya Bajeti imeelezea kwamba, kuna wakati fedha hazikupelekwa MSD kwa sababu ya wizi uliokuwa unatokea pale MSD. Basi tuwe tunapewa pia mrejesho, chenji, wakati ule walipozuia zisiende; zile ambazo zilizuiwa ziko wapi? Au zimefanya nini? Itakuwa ni vizuri sana tukijua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia Mpango huu, moja kwa moja kwanza, nichukue fursa hii kuuelezea Mpango wenyewe na kuangalia kwamba Mpango huu ndiyo mwanzo, ukiwa ni mwendelezo wa Mpango wa Miaka Mitano ulioanza mwaka 2016/2017, ambao unaisha mwaka 2021 na sasa tunaingia Mpango mwingine wa Miaka Mitano. Katika vipaumbele vya ule Mpango wa nyuma, mojawapo ilikuwa ni kukuza uchumi na kuendelea kujenga msingi wa uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapoongelea msingi wa uchumi wa viwanda, huwezi kuacha miundombinu ya barabara, miundombinu ya umeme, vile vitu ambavyo vitachochea kukua kwa uchumi. Sasa nimepita katika Mpango na tuna miradi yetu ya kimkakati na tuliposema ni miradi ya kimkakati, maana yake ni miradi ile ambayo inajenga msingi ambao utakuza uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tunasema miundombinu ya barabara, miundombinu ya reli na mambo ya umeme. Sasa tuna barabara na tuna miradi ya kimkakati ambayo sehemu nyingine ilikuwa inatupelekea kuingiza mapato zaidi au kuongeza pato zaidi la Taifa ambalo lingeweza kufufua sekta nyingine za viwanda. Kwa hiyo, tuna barabara kwa mfano, tuna miradi ya utalii kama ambavyo katika Mpango wake anasema; kukuza utalii ili kuongeza pato la Taifa na tunajua Ilani ya CCM inatutaka tuongeze pato la Taifa kufikia dola bilioni sita ifikapo mwaka 2025. Pia tuongeze watalii wafike milioni tano ifikapo mwaka 2025 na tunategemea sana kutanua uwanda wetu wa utalii ikiwepo utalii Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mbuga kubwa ambayo ni ya pili Afrika ambayo ni Ruaha National Park. Tunaposema utalii wa kusini, unachukua Mikoa yote ya Kusini. Tunaiona Katavi, tunaangalia Kimondo cha Songwe, tunaangalia Njombe Kitulo, tunaangalia Selous, tunaangalia ule utalii wote wa kusini pamoja na Ruaha yenyewe. Sijaona kama Serikali imeweka kwenye Mpango suala la kutengeneza barabara zinazoingia kwenye ile Mbuga. Zaidi sana naona shilingi bilioni 90.2 ambayo itashughulika na miundombinu kufidia hasara zilizotokana na Uviko kwenye Mashirika yale yale ya Utalii kama TANAPA na wengine, lakini hatuoni Mpango ukituambia kuna kutengeneza zile barabara zinazoingia kwenye ile Mbuga ili watalii wanapofika waweze kuingia kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna barabara ile kuanzia Iringa, kilomita 104 kuelekea Ruaha. Tuna barabara nyingine ambayo inaanzia Iringa pia inaingilia Idodi Jimbo la Isimani huko. Hatuoni kama Serikali ina Mpango, zaidi sana waliweka Mpango wa kutengeneza madaraja. Sasa tunatengeneza madaraja wakati sehemu nyingine za barabara ni mbovu. Hii ni miradi ya maendeleo ambayo ingechochea uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, tunaishukuru sana Serikali kwa namna ambavyo inaonyesha uchumi wetu wa Tanzania, pamoja na athari za Uviko bado uchumi wetu umekua chanya. Tusipojiangalia, sisi ni nchi mojawapo katika nchi 11 zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara ambazo uchumi wake unakua kwa chanya. Nchi nyingine zote 33 zinakua hasi, ukiondoa Gabon na ile Afrika ya Kati ambayo uchumi wake ni zero. Sasa tusipojiangalia tulikuwa tunakua uchumi chanya, lakini tutakuja kupitwa na wale waliokuwa na uchumi hasi, kwa sababu ya (nitumie neno lile lile) utelezi ambao tunauweka wenyewe kwenye mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kurudia hapa ni hiki hapa; moja ya sababu kubwa ya kufanya uchumi ukue hasi au kushuka kwa uchumi imeonekana ni Uviko na sababu zilizosababisha ni kufungwa kwa uzalishaji kwenye nchi nyingi kwa jina la kuaminika ambalo lilikuwa ni lockdown. Sisi Tanzania Mwenyezi Mungu alitusaidia tukiwa na Serikali yetu mahiri na shupavu, hatukuwa na lockdown, lakini viongozi wetu walifuatilia ile misingi ya afya tukaweza kuwa salama, tukaendelea na uzalishaji na uchumi wetu ukaendelea kukua katika hali ya kuwa chanya, siyo hasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine kilichoathiri; kwa nini sisi tulikuwa tunaendelea na shughuli za uzalishaji? Kwa sababu, kwa kawaida pia linapotokea tatizo ni fursa, ni mwanya pia wa kuendelea kiuchumi. Kama ninyi ambao mtakuwa mmejipanga vizuri mnaendelea kuzalisha, mngeweza kuwa-serve wenzenu wengine ambao walikuwa wamejifungia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru sana. Basi naomba kuunga mkono hoja. Mengine nitachangia kwa maandishi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwa kunipa nafasi nichangie lakini nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya hasa ya kupeleka fedha nyingi kule chini kwenye grassroot kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie jukwaa hili na nafasi hii kipekee kabisa kuwashukuru sana Watanzania wanaolipa kodi kwenye Taifa letu. Tumeambiwa takwimu zao kwamba ni wachache sana lakini wanabeba mzigo mzima wa watu milioni 61 na sisi tuna walipakodi tumeambiwa walioandikishwa hapa milioni nne na wanaofanya vizuri wapo. Nichukue nafasi hii niwashukuru sana Watanzania mnaolipa kodi kwa ajili ya Taifa letu. Kama unaona kuna mtoto anakwenda shule, kuna hospitali zinajengwa, kuna barabara zinajengwa ni kwa sababu yako wewe Mtanzania unayelipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna hiyo nitoe wito kwa Watanzania wengine na sisi tujisikie wivu kuchangia maendeleo ya Taifa letu. WHO wameainisha maeneo ambayo yanaweza yakasababisha tuka-improve biashara au tukafanya biashara zetu zifanikiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa wanasema lazima tuweke mazingira mazuri kwenye biashara. Hawa Watanzania milioni nne wanaolipa kodi hebu tuwawekee mazingira mazuri tuwaheshimu, tuone kwamba jambo wanalolifanya kwenye Taifa hili ni kubwa sana. Kwanza tunapoweka mazingira mazuri tutaweza kukuza biashara, tutakuza uwekezaji, tutakuza ajira lakini tutajiletea maendeleo ya Taifa letu na wanaendelea kusema kwamba yapo mazingira tunayotakiwa kuongelea ambayo tutatakiwa kuyaweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuwe na mazingira huru ya biashara, tuwe na kanuni nzuri rafiki kwa ajili ya wafanyabiashara, tuwe na soko huria lakini tuwe na mipango ya kutafuta masoko mapya na kukuza masoko tuliyonayo. Kubwa zaidi tuwe na mipango ya kuwahakikishia wafanyabiashara mazingira mazuri ya kufanya biashara. Hapo ndipo tutakapoongeza hiyo tunasema tax base yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea suala la kuongeza au kutanua masoko tumeshaambiwa hapa. Tumeona kazi moja tu ambayo Mheshimiwa Rais ameifanya ya Royal Tour, namna ambavyo imeongeza fursa mpya katika soko letu la utalii ilivyotanua soko letu la utalii na kuvutia utalii. Sasa tunatamani katika hiyo hali na sekta nyingine ziige ili kuweza kupalilia kile ambacho Mheshimiwa Rais amekifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema kwamba tunataka kuweka mazingira mazuri, tuongee tu kwenye utalii. Leo watalii wameongezeka lakini watalii wakija kutalii wanapenda wapate huduma stahiki, wanapenda wale bata. Leo watalii wetu wakiingia Tanzania hata uwezo wa kupata kubadilisha fedha za kigeni ni shida kutokana tu na kutokuwa na maduka ya fedha za kubadilisha yaani maduka ya kubadilisha fedha za kigeni hakuna. Taarifa inasema hapa mpaka Mei, 2023 tayari tuna maduka ya fedha tuliyoyasajili 11. Kule wakati kwenye semina tuliambiwa ni maduka nane yenye matawi 36. Kutoka kwenye Bureau de Change tulizokuwa nazo 2019, 400. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii wazungu wakija Iringa hawana kwa kubadilisha dola ili waende wakale bata Ruaha. Sasa wale Mama aliokwenda kuwaita wanakuja, wanakuja huku wanakutana na broke hakuna pa kubadilisha fedha za kigeni wanarudi mwaka mwingine? Hayo ndiyo mazingira lakini kilichosababisha ni kutokuwa na kanuni rahisi za kufanya biashara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo naona kwanza kwenye biashara hii kuna ubaguzi. Huwezi kuniambia umewapa watu leseni nane wana matawi 36 nchi nzima. Wenye capital requirement ya shilingi bilioni moja moja mmeanza kutubagua Watanzania kwa kuwapa fursa za kufanya biashara kwenye nchi hii watu wenye uwezo wa fedha. Tusio na uwezo wa fedha maana yake tusiwekeze wenye mitaji yetu midogo midogo. Hao mabilionea ndiyo wawekeze. This is not right! Lazima Watanzania wapewe fursa sawa ya kufanya biashara, huo ni ubaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kujenga imani kwa wafanyabiashara ni pamoja na kauli za viongozi kuzingatiwa. Watanzania wana imani kubwa sana na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Leo hii kama Rais atatoa kauli au atatoa maelekezo kwa idara yoyote au Wizara yoyote ya Serikali isipozingatiwa ni kumdharau Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo Watanzania watamwamini nani? Hata Mbunge nikaenda kusema kuna mpango mzuri huu hapa, kama Rais alitoa kauli haikuzingatiwa haikufanyiwa kazi, tunapoteza imani kwa wafanyabiashara kuendelea kuwekeza. Leo tuliambiwa kodi za miaka mitano Rais kasema miaka mitano ya nyuma, miaka sita zisichajiwe lakini hakuna lolote lililofanyika kwenye Mamlaka zetu kuhakikisha hilo halifanyiki na sana sana ukienda wanasema sisi tunasimamia sheria. Nchi hii Watanzania watamsikiliza nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Rais anapokuja anapotoa maagizo anakuwa ameshafanya tit for tat amejua hili linatakiwa mabadiliko ya haraka lakini haya mambo hayafanyiki ndiyo kuweka ugumu kwenye mazingira ya biashara. Watu wanashindwa kutanuka, watu wanashindwa kuwekeza kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ahadi za viongozi zitekelezwe. Mheshimiwa Waziri wa Fedha pale Iringa mwaka jana mwezi wa nane saa hizi tunakaribia mwaka mzima Mheshimiwa Rais alisema na kupitia wewe kinywa chako Mheshimiwa Waziri naongea na Mwenyekiti lakini kwa maelekezo ya Spika kwamba shilingi milioni 700 tutapewa kwa ajili ya kutengeneza mazingira ya machinga. Wale machinga wakiwezeshwa kwenye mazingira yao hayo madogo wata-graduate watakuwa wafanyabiashara wakubwa kuja kuungana huku kwenye shilingi milioni nne. Tukiwawekea mazingira saa hizi ya kumaliza mitaji yao na kuua mitaji yao hatutapata wafanyabiashara wengine wanao-graduate kuingia shilingi milioni nne. Waongeze idadi ya shilingi milioni nne ifike sita wote wanatakiwa watoke huko kwenye biashara ndogo. Kwa nini tunashindwa kuona umuhimu wa kuwatengenezea mazingira mazuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Mheshimiwa Waziri amesoma taarifa yake hapa kwamba anaziwezesha benki, Tanzania Postal Bank na ile benki nyingine wanazipa mitaji lakini kuna benki nchi hii Mheshimiwa Waziri ni community banks, benki ambazo mama ntilie wamechanga hela zao wamepata mtaji wamefungua community bank kama Mkoba Bank ya Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo TRA mmewachukulia shilingi milioni 600 kutoka kwenye account yao kwamba wanadaiwa kodi za miaka hiyo ya nyuma sita, saba huko. Shilingi milioni 600 za mama ntilie wa nchi hii. Hivi Tanzania sisi huwa hatusamehewi kweli madeni huko na mataifa makubwa? Sisi tunakosa kuwasamehe mama ntilie unakwenda ku-freeze account yao, shilingi milioni 600 mama ntilie waliochanga wakaanzisha community bank yao kwa mtaji wao Benki ya Mkoba Tawi la NMB Mkoa wa Iringa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipotengeneza mazingira dunia hii kila nchi inatengeneza destiny yake yenyewe. Tunaongea haya maneno ili wenzetu wayafanyie kazi. Kama benki nyingine unazipa mtaji unaziwezesha, kwa nini community bank usizisamehe madeni yao hii ili wale wakinamama waendelee kukopeshana wenyewe? Tusipoangalia tunapigana wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu kingine ni cha mwisho. TRA nawaomba sana TRA wao ni Watanzania wanapata mental health bila sababu za msingi. Wanakuwa hawana afya nzuri za akili bila sababu za msingi wanakuja kustaafu wanakufa mapema bila sababu za msingi. Wanakosa marafiki mitaani bila sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiajiriwa TRA siyo kwamba umepewa kazi ya kutoa roho za watu. Salimia watu tengeneza mazingira mazuri, hawa Watanzania unayekuwa umemnunia unampa hiyo waliyosema Mheshimiwa Nyamoga lazima alipe shilingi 200,000 lazima akulipe wewe shilingi 50,000 ndiye aliyekuajiri, ndiyo anayekulipa hapo mshahara na kodi yako.

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: …Kwa nini usimhudumie vizuri umbambikize kodi kwa sababu hajasoma halafu unakuja unasema usipojua sheria siyo sababu ya kutosamehewa sheria? Wewe ulisomeshwa na kodi yake ili umsaidie kumuelimisha. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Jesca.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru kwa kunipa nafasi. Nitaanza na Wizara ya Miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niishukuru Serikali kwa kazi kubwa inayofanya katika kutujengea miundombinu. Lakini ninaomba tu, tulikuwa tumepitisha hapa mpango wa miaka mitano na tukaomba wenzetu waweke kipaumbele katika kuimarisha miundombinu inayoelekea kwenye miradi ya kimkakati ikiwepo Ruaha National Park.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani sisi Iringa tupo tayari kuwajaza dollar, kuwajaza pound sterling, kuwajaza ma-euro, lakini utelezi unatokea Wizara ya Miundombinu. Tunaomba barabara zile zinazoinga Ruaha National Park zifikike, tujengewe kwa kiwango cha lami. Ili tazalishe madola tutatue matatizo mengine ya sehemu zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naingia Wizara ya Nishati na Madini, nitaanza na Shirika la STAMICO. Tunaomba sana STAMICO tuwapongeze kwa kazi nzuri mnayofanya, na limekuwa ni shirika sasa ambalo linakwenda kujitegemea baada ya kuwa ICU muda mrefu. Lakini sasa tumejitahidi kuweka maafisa madini kwenye kila mkoa, na tumejitahidi kutanua wigo wa ulipaji madini mpaka kwenye madini ya ujenzi, tunasema mchanga, mawe na kokoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana kwenye mchanga, mawe na kokoto wamejiajiri vijana wetu wa hali ya chini sana. tuwaombe sana Serikali muangalie namna ya kuwabeba wale vijana wasije tena wakafukuzwa na ma- tycoon halafu vijana wetu wakabaki tena wanahangaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Posta lifanyiwe rescheduling. Shirika la Posta lipambane kutokana na mazingira ya biashara yaliyopo, tuondoe urasimu. Hawawezi kupambana na Vodacom Tanzania wakati wao bado wana urasimu na mautelezi kibao, mlolongo mrefu wa maamuzi, timing inakuwa iko nyuma, wafanyakazi wanalipwa bila kuangalia marupurupu kutoka na kwenye industry. Wajitahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANESCO; TANESCO tunaweza tukailaumu sana lakini wafanyakazi wa TANESCO na TANESCO yenyewe siyo kwamba wanawajibika wako kutengeneza umeme kwenye nchi hii. Lazima Serikali iwawezeshe. Tuliwaambia TANESCO wasambaze umeme kwa 27,000 wakati hatujawapa hela yoyote ya kusambazia umeme huo, wakati tunajua vijijini wao wanasambaziwa kwa fedha inayokatwa kwenye mafuta kutoka kwenye REA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANESCO walijiongeza. Inawekezana fedha za kukarabati mitambo wakatumia kupeleka umeme kwa wananchi. Sasa mitambo imeshindwa kukarabatiwa ndiyo inatokea kwamba umeme unakatika kila wakati. Serikali iliangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna ishu ya Kitengo kinaitwa TEITI. TEITI ni Kamati ya Usimamizi, Uhamasishaji, Uwazi na Uwajibikaji kwenye Sekta ya Madini, Mafuta na Gesi Asilia. Kazi yake kubwa ni kutuweka wazi kupitia mikataba, kuangalia mapato ya madini yanayopatikana kwenye nchi yametumikaje kwa maslahi mapana ya wananchi. Yapo maswali mengi sana kwenye jamii, kila ukitaka kuwaambia jamani tuchangie hiki wanakwambia ninyi mna madini, mna gesi, kwa nini hamuwezi kutumia hizo fedha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa TEITI ni kitengo ambacho kinaweza kutusaidia na kipo rasmi kwa ajili ya kazi hiyo. Lakini TEITI ina changamoto, watumishi wa TEITI wako saba wakati TEITI inakitaji kuwa na watumishi 60. Tunategemea hawa wakaangalie uwajibikaji, wakaangalie uwazi kwenye madini, wakapitie mikataba, watuelimishe wananchi mapato tuliyopata kwenye madini, kwenye mafuta, kwenye gesi asilia – watumishi saba. We are not serious. Kwa hiyo tuwasaidie TEITI ili waweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini na bajeti yao iongezwe. TEITI leo tumewatengea milioni 443, wakati hata watu wa nje wanaotusaidia, wale wahisani, wameona TEITI kazi yake ni nzuri, wamewatengea bilioni moja na milioni 725 na wameshalipa, wameshawapa nusu ya hiyo fedha. Na sisi tumewapa milioni 200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kupunguza maswali mengine yasiyokuwa na msingi; madini mnatumiaje, mapato ya gesi yanatumikaje, mapato ya mafuta yanatumikaje. Taasisi kama hizi ambazo tumeziunda zifanye kazi. TEITI inatakiwa iwe na wajumbe nane wa kutoka kwenye Wizara wanne, lakini wanaotoka kwenye NGOs wale wanaharakati wa kupigania mapato ya wananchi wawili na wengine wanatoka kwenye makampuni hayo ya mafuta na gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni shirika la Uwazi ambalo limekubali na sisi tumeridhia kwa Sheria Na. 23 ya mwaka 2015 ambapo tumeungana na mataifa mengine yenye rasilimali hizi za madini, mafuta na gesi ili kuweka uwazi. Sasa basi tuwasaidie TEITI waweze kufanya kazi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia kwa kusema ndugu zangu, Wizara ya Miundombinu msitupe utelezi. Tunaomba lami tuwajaze madola na mayuro, Iringa tuko tayari jamani. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, location ya Jimbo la Manispaa ya Iringa, lipo katikati ya majimbo mengine ya Mkoa wa Iringa, hivyo kusababisha watu kutoka katika Mkoa wote wa Iringa kuona urahisi wa kufuata huduma za muhimu ndani ya Manispaa ya Iringa. Hii imesababisha uhitaji wa huduma za jamii kama afya, elimu, miundombinu ya barabara kuwa changamoto, kwani tunalazimika kuhudumia watu wengi zaidi ya wakazi waliopo ndani ya mji. Mfano Hospitali za Wilaya za Jimbo la Kilolo imejengwa Wilayani Kilolo ili watu wafuate huduma hiyo Kilolo wanatakiwa kupita Manispaa ya Iringa.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa hali ya kawaida hawezi kupita mjini kwenda kuifata hospitali iliyoko Kilolo. Wanatakiwa kutibiwa Manispaa, jiografia hiyo iko pia kwa Jimbo la Isimani na Kalenga.

Hivyo tuna umuhimu wa kuongeza vituo vya afya pembezoni mwa Jimbo la Iringa, ambayo ni Kata ya Kitwiru, Kata ya Igumbiro na Kata ya Isakalilo. Pia utanuzi wa Hospitali ya Frelimo uende kwa kasi na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa ili kuhimili uhitaji uliopo.

Pia shule kongwe kama Iringa Girls, Lugalo Sekondari na Mawele Wele Sekondari, ziongezewe mabweni kwa kuwa ni shule za kitaifa halafu zinachukua watoto wenye ulemavu wa kila aina. Sasa zinazidiwa sana wakati zina maeneo ya kutosha kufanya expansion. Iringa Girls imaliziwe yale mabweni mawili ambayo hayakumaliziwa wakati wa ukarabati wa shule kongwe ambayo ni bweni la Mshikamano A na B.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa madarasa kwenye maeneo yetu uzingatie uhitaji, kuna sehemu nyingine shida kubwa inakuwa sio tu madarasa bali majengo mengine. Pia fedha za ujenzi wa mabwalo ziangaliwe upya na zitolewe sawa kati ya TAMISEMI na Wizara ya Elimu, wengine wanatoa chache wengine nyingi, baadhi mabwalo yanaisha kwingine inashindikana. Ndani ya Manispaa tunaomba mabwalo yamaliziwe katika sekondari zetu ambayo hayajakamilika. Kama Kwakilosa Sekondri, Mlandege Sekondari, Tagamende Sekondari na kadhalika.

Pili, Iringa Manispaa imekuwa na shida kubwa ya mara kwa mara vifungu ku-burst hivyo kusababisha uendeshaji wa halmashauri kuwa mgumu na kuwakosesha Madiwani kulipwa posho za vikao kwa wakati na kuwalipa wazabuni wa Manispaa na kuendesha shughuli nyingine, hili lifanyiwe kazi.

Mheshimiwa Spika, pia ulipaji wa madeni makubwa kama deni la Kampuni ya SIETCO, wanaoidai Manispaa pesa za ujenzi wa stendi ya Igumbiro na soko la Mlandege vilipwe ili kuondoa hasara ya kulipa penalt na kuja kuzuia wahisani kutoa misaada pia.

Mheshimiwa Spika, TARURA tunaomba sana kwa namna Mji wa Iringa ulivyokaa, unapitiwa na barabara kubwa za kimataifa mbili (TANZAM). Iringa Manispaa inapitiwa na barabara kubwa ya kutoka mikoa kumi ya Kusini kwenda Mashariki ya nchi yaani Mbeya – Dar es salam; pia inapitiwa katikati na barabara inayotoka Cape Town to Cairo yaani mikoa 10 ya Kusini mwa Tanzania ikiwemo Nyanda za Juu Kusini kwenda mikoa sita ya Kanda ya Ziwa na Kaskazini mwa nchi mikoa sita. Sasa jaribu kufikiria huo mzigo unaopita Iringa wakiwemo na wakazi kutumia barabara hizo hizo. Ni shida kubwa sana na kumekuwa kuna mkwamo na ajali nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, tunaomba barabara za ndani za Mji na Manispaa ya Iringa zijengwe kwa kiwango cha lami ili kuufungua mji ule ili angalau wanancchi watumia barabara za pembezoni ili kupisha watumiaji wa Kimataifa watumie hizo nyingine. Mfano barabara ya Ipogolo – Kagrieolo - Kitwiru; Wilolesi - Mtwivila; Magereza - Ipogolo; Don Bosco - Kihesa Kilolo kupitia Magic Site, pia kukamilishwa kwa Iringa bypass.

Mheshimiwa Spika, otherwise tunawashukuru sana kwa juhudi kubwa na kazi inayotukuka inayofanywa na TAMISEMI kwa ujumla.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Iringa ni mkoa wa kilimo hususani hata Manispaa ya Iringa. Sasa sisi hatuna eneo la kufanya block farming na Iringa Manispaa ndiyo lango la utalii Kusini na tunajengewa uwanja wa ndege ambao utaruhusu hata ndege ya mizigo kutua na kuchukua kama mboga mboga.

Mheshimiwa Waziri wewe unajua utalii ni pamoja na huduma nzuri ya chakula. Hivyo basi, rejea mazungumzo yetu, tunaomba sana sana tupewe eneo la Serikali lililokuwa la Kilimo au Utafiti Gingilanyi, katika Kata ya Nduli ili tutumie kama block farming kwa vijana wa manispaa ya Iringa, pia tunaweza tukatumia eneo lililokuwa Kituo cha Utafiti cha Kilimo kilichopo Ipogolo Kata ya Ruaha.

Mheshimiwa Spika, pia tunaeneo la umwagiliaji la Mkoga Kata ya Isakalilo. Tunaomba litengewe bajeti kwa ajili ya kuboresha ili kuwa na kilimo cha umwagiliaji na chenye tija.

Mheshimiwa Spika, tunaomba changamoto ya upatikanaji wa mbolea karibu na wakulima itatuliwe, kwanza, kwa kuweka mfumo madhubuti ambao utafanya kazi kwa wakati wote bila kukatikakatika, kuwa na wasambazaji wa kutosha mpaka vijijini hivyo kuimarisha utendaji kazi wa mawakala wadogo kwa kuondoa urasimu usio kuwa wa msingi kwa mawakala wadogo. Pia kuufanya mfumo usiruhusu QR code kuwa scanned zaidi ya mara mbili, iwe kama ilivyo kwenye voucher za simu au namba za LUKU ukiingiza mara moja haiwezi kuruhusu tena kuingiza au ku- scan. Pia zisitolewe zinazofanana kwa makampuni mawili.

Mheshimiwa Spika, mbolea hii ya ruzuku ikiwezekana iwe na limit ya mifuko itakayotolewa. Labda Serikali iseme itatoa ruzuku kwa mifuko kadhaa tu. Wale wenye mahitaji makubwa maana yake wana uwezo mkubwa hivyo waweze kununua kwa bei ya kawaida isiyokuwa na ruzuku. Wakulima wakubwa wengine huchukua mbolea ya kutosha wakulima wa Wilaya nzima hawa wanaweza. Mbolea ya ruzuku itolewe kwa mwaka mzima. Pia usajili wa wakulima kama wapo ambao bado hawajamaliza basi waendelee kutumia mpaka wamalize na usajili wa wakulima uwe ni endelevu.

Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze kwa kazi kubwa inayofanywa na Wizara ya Maji chini ya Waziri Aweso, kipekee sana kwa heshima na taadhima wananchi wa Iringa tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa unayofanya ya kuliongoza Taifa letu, na kusimamia maendeleo ya Taifa letu, na hususani katika Manispaa yetu ya Iringa. Tunashukuru kwa kuwa maji ndani ya Jimbo la Iringa imekidhi utekelezaji wa Ilani.

Mheshimiwa Spika, maombi; kwanza, tunaomba maji yafikishwe kwenye maeneo ya vijijini ndani ya Jimbo la Iringa ambayo ni eneo la Ugele, Kata ya Mkimbizi na Mosi Kata ya Kitwiru. Pia ninaomba kisima katika eneo letu la Uwanja wa Samora pale tulipofanyia mkutano ulipotuahidi kutuletea visima, siku ya ziara ya Rais, pamoja na zile shule tulizoomba kuchimbiwa visima.

Mheshimiwa Spika, Mkurugenzi wako IRUWASA amesema maji yapo kwenye shule hizo, na wamefungiwa prepaid, lakini hawatumii kwa kuwa bills hawawezi kulipia.

Pili, ninatoa ushauri kuwa katika bill ya maji muongeze hata shilingi 10 au tano kwa unit ili fedha hizi zichangie huduma za maji mashuleni, kwenye zahanati na vituo vya afya. Shule hizi zinawekewa miundombinu ya kisasa sana inayohitaji matumizi ya maji. Sasa kutegemea capitation pekee yake itakuwa vigumu sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe shukrani za dhati kwa Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kazi kubwa wanayofanya ya kulinda raia na mali zao. Hata hivyo nina mambo kadhaa ya msingi sana ya kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu kuwajumuisha polisi kutumia kikokotoo kama watumishi wengine wa Serikali tofauti na askari wengine wa majeshi mengine. Yapo malalamiko makubwa miongoni mwa askari kutoridhika na utaratibu huo. Askari hawa wa Wizara hii wanaona ni vyema utaratibu unaotumika kutoa mafao au kikokotoo kinachotumika kwa askari wengine mfano toka Wizara ya Ulinzi utumike na kwao pia kwani mazingira yao ya ufanyaji kazi yanalingana na askari wengine, lakini pia hawana muda wa kufanya mambo yao wanapokuwa katika ajira ukilinganisha na watumishi wengine wa umma, hivyo hawana muda wa kutafuta fedha nyingine kwa ajili ya kujiandaa na maisha ya kustaafu kama ilivyo kwa watumishi wengine wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia viinua mgongo vyao au pensheni zao kwa walio wengi sio kubwa, hivyo, kutumia kikokotoo cha asilimia 33 hakiwasaidii kujiweka vizuri kwa maisha ya kustaafu, na pia umri wao wa kustaafu ni tofauti na wastaafu wengine wa kada nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ni vyema kwa ufanisi bora wa majukumu yao wakiwa na afya nzuri ya akili wawapo kazini na baada ya kustaafu, tunaiomba Serikali ilipe uzito jambo hili la kutumia utaratibu wa kuwalipa mafao kama askari wengi wa Wizara ya Ulinzi na sio kikokotoo hiki cha asilimia 33 kama kinavyotumika kwa watumishi wengine wa umma ili kuweka heshima sawa kwa askari wetu wote na kuimarisha usalama wa raia na mali zao.

Pili, Serikali iweke mpango mahususi kwa kutumia nguvu kazi yake wakiwemo wafungwa na mahabusu kuhakikisha inaboresha makazi ya askari. Mfano makazi ya askari polisi ndani ya Jimbo la Iringa hayaridhishi. Hata makazi ya askari polisi wa Dodoma Kituo Kikuu cha Polisi Iringa Road hayaridhishi, ni aibu kwetu kama viongozi kuridhika kuwa na makazi duni namna hii ya askari wetu ambao ndiyo wanalinda mali na wananchi wetu wote yakiwemo mahoteli makubwa, maghorofa na roho zetu Watanzania wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, wenza au wanawake wa askari polisi waangaliwe kwa namna ya kipekee katika kuwawezesha kiuchumi ili kusaidia ustawi wa familia za askari wetu. Kwa kuwa mara nyingi kupata ushirikiano wa kukopeshwa kwenye vikundi mitaani inakuwa ni changamoto kutokana na kazi za wenza wao. Uwepo mpango mahsusi wa kuzisaidia familia za askari kiuchumi kwa kuwawezesha wenza wao.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ione namna ambavyo itakuza utamaduni kwenye maeneo ambayo yanapakana na mbuga zetu au maeneo ambayo watalii wengi hutemebelea kwa nia ya kusaidia kukuza utalii na kuongeza ajira nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Iringa kama lango la utalii liangaliwe pia hasa ukizingatia historia ya watu wa Iringa na Chifu Mkwawa. Pia kuanzisha matukio mbalimbali kama mashindano ya ngoma, mbio na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara ibuni njia muhimu za kushirikiana na wadau kuinua utamaduni wa sehemu husika na kuibua vivutio mbalimbali vilivyopo kwenye miji nchini ili kuimarisha ustawi wa afya ya jamii miongoni mwa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika kulipongeza Jeshi letu kwa kazi kubwa wanayofanya, hasa kuhakikisha usalama wa nchi yetu na ulinzi wa nchi yetu tunakuwa salama sana.

Mheshimiwa Spika, leo ningeomba niongelee kipengele cha JKT, yapo mambo mengi yanatuumiza akili, tunachanganyikiwa hatujui tunafanya nini, kumbe tuna vyombo humu ndani ambavyo hatujavitumia sawa sawa na kama tungevitumia matatizo yetu makubwa yanayotukosesha usingizi, mambo kama ajira kwa vijana, mambo kama maadili kwenye Taifa letu, mambo kama uzalendo, mambo kama ukakamavu, tayari tungekuwa tumeweza kwa kiasi kikubwa sana kuyatatua.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri amesoma utekelezaji wa Ilani kile kipengele (H) na wote hapa tupo kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, na Chama cha Mapinduzi kina viongozi makini wenye uelewa mkubwa wanaoona mbali sana. Wametuelekeza au wamekuelekeza Mheshimiwa Waziri katika utekelezaji wa Ilani (H), kuimarisha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Kujenga Uchumi (JKU) ili viwe vyombo vya kuwapatia vijana ujuzi wa kujiajiri na kuajiriwa na pia kuwa vyombo mahiri vya huduma na uzalishaji mali hasa katika ujenzi wa kilimo, ufugaji, uvuvi na maeneo mengine. (I) inasema hivi, ili uweze kutekeleza hilo (H) lazima sasa kupanua na kuongeza idadi ya Kambi za JKT na JKU. Ili kuwezesha vijana wengi zaidi, wakiwemo wahitimu wote kwa sababu JKT ina makundi mawili ya vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna vijana tunawachukua kwa mujibu wa sheria na tunao vijana tunaowachukua kwa kujitolea. Wale wa kwa kujitolea ndiyo Ilani inasema kuwawezesha wengi, wale wa mujibu wa sheria Kidato cha Sita ni wote. Utalitekelezaje hili lazima uhakikishe kwamba unapanua na kuongeza Kambi za JKT na JKU.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ukisimama hapa utuambie safari hii unafanya nini katika kuongeza makambi, tunataka vijana wote wanaomaliza Kidato cha Sita waende JKT. Tunataka uongeze idadi ya vijana walioko mitaani waende JKT, kwa sababu JKT kwanza ina majukumu, objectives zake iliyopewa. Objective ya JKT namba moja ni malezi kwa vijana wetu, objective nyingine ni kuzalisha mali, kuwafundisha vijana wetu kuondokana na mentality ya kufikiria kwamba kazi za ofisini ni bora kuliko kujiajiri, kuzalisha mali lakini ni ulinzi wa Taifa letu. Kutoa mafunzo ya uhakika kwa vijana wetu kuhakikisha kwamba wanakuwa wazalendo, wakakamavu, kuendelea kulinda Taifa letu. Malezi ya vijana, kuwa na vijana wenye nidhamu, wakakamavu, wenye kujitegemea, wenye uwezo wa kufanya kazi ili kuleta maendeleo kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumbe ni wakati muafaka sasa kama alivyosema kaka yangu Mheshimiwa Kingu, kumbe Wizara nyingine hizi zilitakiwa zifanye coordination na JWTZ na JKT kupeleka programu zao waseme sisi tunayo programu ya kuwafundisha vijana kupitia BBT hawa hapa. Kwa sababu Mheshimiwa Waziri kinachosumbua sasa hivi kwa vijana wetu, shule tumejenga nyingi, vyuo vingi ujuzi wanao, kinachosumbua ni ukakamavu, ni nidhamu na kujitegemea, hivi watavipata kule! Tunao Maafisa Kilimo yes, tumewadahili kwenye vyuo vya kilimo lakini Afisa Kilimo anaogopa nyoka, na nyoka wanaishi mashambani, akapate ukakamavu jeshini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tuna vijana tumewafundisha sasa hivi tumewapelea BBT watajifunza vizuri na mimi nashukuru nimetembelea kituo kimoja wanafanya vizuri lakini akishika jembe, akinyanyua tu jembe analiangusha lina mkata, ukakamavu haupo. Tunao vijana wengi tunawafundisha au tunawadahili wanakwenda vyuo vikuu wanamaliza form six, wanakuwa wasomi wazuri, madaktari wazuri lakini uzalendo hakuna. Mtu anaona bora mgonjwa afe yeye akimbie na dripu akauze. Kwa hiyo, kumbe mwarobaini wetu ni JKT na wazazi wetu waliliona hilo na ndio maana nikawa najiuliza ni kwa nini Waziri Mkuu Hayati Rashidi Kawawa aliamua kwenda JKT, ni kwa nini Mzee Aboud Jumbe aliamua kwenda JKT, ni kwa nini Mzee wangu mimi Adam Sapi, Spika wa kwanza wa Bunge hili aliamua kwenda JKT. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule ndiko alikopata uzalendo na ukakamavu, wakajifunza nidhamu, leo tuna vijana tumewaendeleza sayansi na teknolojia Mheshimiwa Nape alikua anazindua minara 700 tunaweka huko lakini wengine wanatumia tu kutukanana au kutukana viongozi wetu au kui - defend Serikali yetu. Tusipowapeleka hawa JKT kujifunza uzalendo haina maana uwekezaji tuliofanya.

Mheshimiwa Spika, Serikali lazima mkae kama kitu kimoja mkubaline kwamba chombo kilichopitishwa kisheria na Bunge Tukufu kwa ajili ya malezi rasmi ya vijana wetu ni JKT, hatuhitaji tu akili za darasani Intelligent Quotient, ukishamjengea mental structure tunahitaji physical structure yake kwenye performance. Ana akili nzuri ni Afisa Kilimo mzuri lakini kuna mahali atatakiwa a - demonstrate ashike jembe achimbe, amuoneshe mkulima namna ya kufanya lazima huyu awe mtu makini, awe mtu mkakamavu, awe mtu mzalendo, awe ni mtu mwenye nidhamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, JKT lazima iwezeshwe Waheshimiwa Wabunge, hiki ndiyo chombo kinachotuunganisha vijana wetu kama Taifa pekee yake. Huku kwingine tukiungana tunaungana kama Vyama vya Siasa, tunaungana kama CCM, tuna green brigade wetu, wanaungana kama CHADEMA wana red brigade. Huku ndiko tunakounganishwa kama Watanzania, tunaongea maslahi ya Watanzania, huku ndiko tunapelekwa bila ukabila, huku ndiko tunakopelekwa bila kujali itikadi za imani zetu. Tunakwenda kuambiwa sisi ni Watanzania we are blessed to be Tanzanians, tunaijenga Tanzania. Vijana wetu lazima wakue na mentality hiyo, wasifikirie tu kuona kwamba nchi zingine wanafanya vizuri, wanaishi vizuri natamani kutorekea huku, natamani kutorekea huku. Haina maana nchi hii, humu humu ndiyo nchi ya asali na maziwa hapa hapa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana JKT, halafu kulala kule JKT namshukuru Mungu alinipa privilege nikaenda. Majengo ya JKT wala hayahitaji gharama kubwa wala is not a mansion kama hili Bunge letu. Wao wanapiga tu yale mahanga, bati na nini na nini, Waziri utuambie ukija hapa, CCM imekuelekeza hapa, wewe unajenga kambi ngapi? Vijana wengi tunataka kuona wanapungua mitaani unaniambia…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Ninataka kuona unanimbia Mheshimiwa Jesca leta vijana toka Iringa tuwapeleke JKT, wakajifunze uzalishaji mali, uzalendo na jinsi ya kulitumikia Taifa na kujitegemea wao wenyewe.(Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Jesca Msambatavangu kengele ya pili imeshagonga.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, kuhusu utalii Kanda ya Kusini (REGROW), utekelezaji wa mradi huu umesaidia kuboresha miundombinu katika hifadhi na utatuzi wa migogoro.

Mheshimiwa Spika, naomba kuipongeza Wizara hii kwa kazi kubwa ya kukuza utalii na maliasili zetu. Pongeza pia za kipekee zimuendee Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mchango wake binafsi katika kuendeleza Wizara hii kupitia Royal Tour.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita katika kujenga kituo cha Utalii Kusini chini ya REGROW kiitwacho Kihesa-Kilolo ambacho kinatakiwa kujengwa katika Manispaa ya Iringa ambalo ni lango la utalii Kusini. Umuhimu wa vituo hivi vya kitalii duniani ni kutoa taarifa na elimu kwa watalii kuhusiana na mwelekeo au ramani ya eneo husika ambalo mtalii anatakiwa kutembelea, kutoa taarifa ya huduma zilizoko katika eneo hilo la utalii, ni sehemu inayomuunganisha mtalii na eneo la utalii. Hivyo basi, ni lazima tukubaliane kuwa pamoja na uboresha mbalimbali unaofanyika kwenye mbuga na hifadhi zetu, bado tujue ni muhimu sana kuwa na kituo cha utalii au information centre ambacho ni Kihesa Kilolo.

Mheshimiwa Spika, Kituo hiki kitatakiwa kutoa taarifa za Utalii Kusini yote, sio Iringa pekee yake. Utafiti unaonesha ili tufikie lengo la Ilani yetu ya kufikia watalii milioni tano ifikapo mwaka 2025; basi ni muhimu kujenga kituo hiki. Sababu ni kwamba huwezi kupeleka watalii wote hawa Kaskazini, utaharibu kabisa ikolojia ya utalii wenyewe Kaskazini. Tabia za watalii hutaka kupata taarifa mapema kutoka kwenye vituo hivi kabla hawajaanza safari ya kutembelea eneo husika. Sasa kwa wale wanaotaka kuja Kusini wanapata taarifa wapi?

Mheshimiwa Waziri, msiseme tu muda unaturuhusu mpaka mwaka 2025, utakuwa unaenda kinyume na Mpango wa Miaka Mitano na Ilani ya CCM, inayotutaka tuongeze pato la Taifa. Mchango wangu namba mbili, moja ya sababu kubwa inayowafanya watalii kutorudi nchini ni kukosekana kwa huduma bora muhimu ikiwepo, kupatikana kwa fedha za kigeni. Mheshimiwa Waziri fanya jitihada zako binafsi bila kuwategemea Wizara ya Fedha kuhakikisha, maduka ya fedha za kigeni yanarudishwa nchini, hasa maeneo ya utalii. Pigania Wizara ya Fedha kupitia BOT waondoe masharti yasiyokuwa rafiki yanayosababisha maduka ya kubadilishwa fedha za kigeni yasiwepo.

Mheshimiwa Spika, tatu, Iringa Mjini kama lango au reception ya Utalii Kusini, lazima sasa tukuombe Mheshimiwa Waziri kuweka msukumo mahsusi wa kuwaandaa watu wa Iringa kuwa wakitalii. Mamlaka za Iringa kuwa kitalii, mazingira ya Iringa kuwa kitalii ikiwemo kuhakikisha misitu ya asili inalindwa kwa kushirikia na programu za TFS, kama kupanda miti, kutunza miti ya asili, kutoa mizinga ya nyuki ili kupunguza ukataji wa miti hovyo kuifanya Iringa kwa Southern Geneva); ikiwemo kuanzisha zoo, hili mimi mwenyewe naweza kusaidia.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapo wind-up atoe kauli thabiti amejipanga vipi kuwafanya watu, viongozi, mji wa Iringa, mazingira ya Iringa kuwa ya kitalii (Southern Geneva of Africa). Naunga mkono hoja naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Mapitio ya Hali ya Uchumi wa Taifa 1.3.1. Pato la Taifa na Ukuaji wa Uchumi katika kipindi cha Januari hadi Septemba, 2022, Uchumi wa Taifa ulikua kwa wastani wa asilimia 5.2 ikilinganishwa na asilimia 4.8 katika kipindi kama hicho mwaka 2021. Ukuaji chanya wa uchumi ulichangiwa na jitihada mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ikiwemo mikakati ya kukabiliana na athari za vita kati ya Ukraine na Urusi; ruzuku kwenye mafuta shilingi milioni 100 kila mwezi, uwekezaji wa kimkakati katika miundombinu ya nishati (trilioni 6.55 limefika 86.89%), maji (trilioni 1), afya (trilioni 1), elimu, barabara, reli na viwanja vya ndege; kuongezeka kwa uzalishaji wa madini, hususan dhahabu na makaa ya mawe na kuongezeka kwa mikopo katika sekta binafsi ambayo imechochea shughuli za kiuchumi.

Aidha, ukuaji huu ulichangiwa na kuongezeka kwa shughuli za utalii kutokana na kampeni ya Royal Tour. Ukuaji huu wa uchumi unaashiria kuimarika kwa shughuli za kiuchumi katika sekta mbalimbali pamoja na kuongezeka kwa ajira na mapato ya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo matatu ambayo yatasababisha Watanzania kuhamisha uwanja wa vita; kwanza Bureau De Change - BoT/masharti ya kuanzisha Bureau De Change yawe rahisi ili kurahisisha upatikanaji wa dola nchini na kukuza utalii; pili, madeni ya kodi za muda mrefu - TRA lifanyiwe kazi; tatu, gawio kwa Watanzania kwenye makampuni ya hisa- kama Vodacom wafuatiliwe ili wawe wanatoa gawio.

Mheshimiwa Naibu Spika, madaraka ya Kamishna ni makubwa mno kiasi cha kukiuka haki za binadamu na baadhi ya sheria hasa Kamishna akiwa negative thinker.

Mheshimiwa Naibu Spika, machinga wa Iringa waliahidiwa na Rais fedha zao shilingi milioni 700; tunaomba Wizara ya Fedha itoe.

Kuhusu utoaji maamuzi chanya kwa viongozi wa juu wa taasisi unazoziongoza uko chini sana, wawe wanatoa maamuzi mapema na kwa wakati ili kuepusha migogoro kama migomo na kufifisha uzalishaji kwa wananchi; kupuuza maagizo ya viongozi ikiwemo Mheshimiwa Rais, mfano kutotoza kodi za miaka ya nyuma na ya muda mrefu, kutorudisha fedha za Bureau De Change na kusingizia Bunge na vyombo vingine vya sheria waache. Wawajibike! Nia ovu isiwepo kama ku-seize fedha za Community Banks kama Mucoba bank milioni 600, ni kutowatendea haki wananchi.
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami nichukue fursa hii kwa kweli kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tuzo hii aliyoipata. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mimi ni Balozi wa Afya ya Akili, nitaomba nitumie mfano ili watu waelewe, kwa sababu kuna watu wengine huwa pia hawaelewi. Mimi niseme hivi, hii tuzo ni kama kombe ambalo huwa zinacheza ligi zetu humu ndani ya nchi. Hapa hii tuzo ilikuwa inagombaniwa na nchi 54. Nchi zote za Bara la Afrika na wachezaji walikuwa ni Wakuu wa Nchi kwenye timu hizo, lakini aliyekuwa kashikilia tuzo hii ilikuwa ni wenzetu Nigeria. Kwa hiyo, naweza nikaendelea kutoa mfano; nichukulie kama Nigeria ilikuwa ni Yanga na Mama Samia ni Simba; wameingia kwenye fainali. Zilikuwepo sheria, kama zilivyo sheria 18. Hapa kamati ile ikaangalia, maana kuna watu hawaelewi wanafikiri labda imetolewatolewa tu kwa sababu ya hivi hivi, hapana. (Makofi/Kicheko/Kigelegele)

Mheshimiwa Spika, jambo mojawapo Mbunge mwenzangu aliyemaliza kusema ameshamaliza. La kwanza, ilikuwa wameangalia shilingi milioni 290 ambazo Tanzania tume-qualify kwa vigezo kupewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika kwa ajili ya kuendeleza miundombinu chini ya usimamizi wa Rais Samia Suluhu Hassan, tukashinda kwa vigezo, tukaonekana tunafaa kupewa fedha hiyo kwa ajili ya kuendeleza miundombinu ya barabara, reli na usafiri wa anga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ya pili ikaangaliwa maono yetu baada ya kuwa tunajenga reli, tutai-manage vipi? Tutaiendeleza vipi? Tukaingia mkataba na kampuni nyingine ya China kutupatia modern flit cars kwa ajili ya kuendeleza sekta hii ya reli ambapo tutakuwa na magari 1,430 kwa ajili ya kusimamia uendelezaji wa sekta hii ya miundombinu ya reli. Hii iligharimu karibu dola milioni 172.2. Hayo ndiyo tuliyomtoa knockout Nigeria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ya tatu, ikaonesha nia ya Serikali ya Rais Samia; nimewahi sikia tetesi tetesi kwamba ule Mji Mkuu wa Nigeria, Abuja ule ramani yake inafanafana na masterplan ya Mji wa Dodoma. Sasa wao wamejenga ule Mji lakini walishindwa kwenye ring road hawajafanya. Sisi Tanzania tarehe 11 Februari, Rais wetu amezindua na kuanza rasmi ujenzi wa ring road katika Mji wetu wa Dodoma. Hiyo moja ilikuwa ni credit. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndugu zangu Watanzania tunaposema Mama anafanya kazi kubwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hata vitabu vya Mwenyezi Mungu vinasema, wakati mwingine Nabii hapati heshima kwao. Ila mimi kama Balozi wa afya ya akili, naweza nikasema ni matatizo pia ya afya ya akili kutotambua kwamba una kitu cha thamani au una kiongozi bora ndani ya nyumba yako na kubeza juhudi za mama anapotoka kwenda kutafuta chakula; au baba anapotoka kwenda kupambana na maisha ili arudi na kitu kuendeleza familia. Ile nayo ni matatizo ya afya ya akili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndugu zangu mama anapokuwa katika harakati za kuwepo ndani ya Tanzania, au anapokuwa katika harakati za kuwepo nje ya nchi ya Tanzania, ni kwa maslahi mapana ya Taifa letu. Leo hii katika hiyo fedha kila Mbunge hapa alipewa shilingi milioni 500 na wengine wamepewa shilingi bilioni moja. Leo hii nikifika Iringa, nikienda katika Kata yangu ya Mkimbizi pale, Namtivila kuna barabara tumejenga ambayo tumepeleka shilingi milioni 500 kutoka katika mgao huu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa, kengele imeshagonga, ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa hiyo, nawaomba ndugu zangu tumuunge mkono mama, anaupiga mwingi!

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pia kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ardhi na nitakuwa na mambo makubwa mawili. Niwapongeze kwanza kwa kazi nzuri pia ambayo wanafanya kwa sababu yapo mazuri mengi pia ambayo wanayafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka kuchangia kuhusiana na mpango wa matumizi ya ardhi na uendelezaji wa makazi. Kama Mbunge mmoja alivyokwishasema hapa; ardhi ni nguzo moja wapo katika nguzo nne ambazo Mwalimu Nyerere alisema, tunahitaji ili tuendelee, kwa sababu kila kitu kinafanyika kwenye ardhi. Sasa basi, kwenye upande wa makazi na matumizi bora nimeona kwamba wanasema mpaka 2025 inatakiwa vijiji vyote viwe vimepima na wamejiwekea namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miji tunayotoka pia kuna maeneo ambayo ni peri urban, haya sijaona mpango wake wamewekaje, yaani kwenye miji hakuna vijiji lakini tuna mitaa, lakini ile mitaa inaitwa mitaa kwa sababu tu ipo kwenye municipals au kwenye majiji; lakini ukiangalia hali halisi ni kama vijiji. Sasa sijui hii inaingizwa kwenye mpango gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni cha muhimu sana kukizingatia kwa sababu inatuletea shida hata kupeleka huduma kama hatuweki huu mpango wa matumizi bora ya ardhi mapema; hata kupeleka huduma kwa wananchi inakuwa ni kazi. Wakati ule Mwalimu Nyerere alianzisha zile program za vijiji vya ujamaa, of course yeye alianzisha kwa sababu ya mambo yake ya ujamaa na siasa za ujamaa na kujitegemea, lakini zilikuwa zina msaada kwa sababu hata wanapopeleka huduma wanawakuta wananchi wapo sehemu moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunataka kujenga barabara, unamkuta mtu alikuwa ni mwindaji, akaenda kuwinda mbali na wenzie, baadaye akajenga nyumba, akaanzisha familia iko mbali sana, sasa kule wanaendelea wanatengeneza familia wapo watu 200, wapo watu 150 kutoka kwa wenzao walipo ni kilometa zaidi ya 70 au 60; Serikali inalazimika kupeleka barabara mpaka kule, kuwapelekea shule lakini hawa watu wangekuwa sehemu moja kwenye kijiji ingelikuwa ni rahisi au kwenye mtaa, ingekuwa ni rahisi ku-concetrate kwamba tunawapelekea mahitaji ya muhimu pale ya huduma; lakini yale maeneo mengine wakatumia kwa ajili ya uwindaji au kwa ajili ya kilimo kama ambavyo wametumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamesema wanaimarisha TEHAMA, naomba katika zoezi la kuimarisha TEHAMA waangalie pia kuwapa mafunzo watu wao wa chini hasa kwenye kada hizi za chini kwenye halmashauri. Nasema hivi kwa sababu wengi, leo ukienda kwenye halmashauri wanatoa risiti za kuwadai kodi za ardhi wananchi ambazo siyo halisi. Ukiwauliza wanasingizia mfumo, wakati mfumo ule anau-feed mtu, hakuna mfumo ambao unajiweka peke yake halafu una generate data peke yake, ni watu ndiyo wana feed zile information kwenye mfumo. Sasa inaonekana watu wanakuwa hawapewi mafunzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine tunaomba kwenye mambo ya MKURABITA, sasa hivi kwenye miji yetu MIKURABITA haipo tena, zile program za MKURABITA za kupima yale makazi ambayo hayakuwa rasmi haziendelei, sasa ujenzi holela unaendelea. Hata hivyo, kipo kipengele waliotoa kwenye Kamati zetu za Mipangomiji, cha kupitisha vibali vya ujenzi, wakaacha inawezekana walikuwa na nia njema kwamba vitolewe kwa wakati, viende na kasi na wananchi kwa sababu zile Kamati zina muda maalum. Hapa nafikiri wanatakiwa warudie waangalie ili kwamba Kamati zile zipewe mandate tena ya kuwa zinatoa vile vibali; kwa sababu tayari katika miji yetu ujenzi holela unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ninalotaka kuongea linahusiana na kodi ya ardhi (land rent) hasa kwenye taasisi; Taasisi za Dini, Taasisi za Shule na Taasisi za Vyuo. Ukiangalia hasa kwenye shule binafsi na kwenye vyuo binafsi. Suala hili limekuwa ni tatizo kubwa lakini katika hotuba ya Mheshimiwa Rais, alikuja hapa tarehe 22 Aprili, 2021, akatuambia kasome ile hotuba yake kitabu chake ukurasa wa 10, paragraph ya kwanza, ya pili mpaka ya tatu; alielezea ni namna gani ambavyo mazingira yetu ya uwekezaji wa biashara hayajaboreshwa; hasa kwenye Sera, Sheria na Kanuni zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, akaahidi katika paragraph ya kwanza kuonesha anaboresha sera, sheria na kanuni. Paragraph ya pili na kuelezea hatua zinatakiwa kuchukuliwa ili kuvutia uwekezaji na sekta binafsi kuwekeza; lakini paragraph ya tatu akasema, nchi yetu imekuwa ikilalamikiwa kwa kutokuwa na mazingira mazuri ya uwekezaji. Kwanza kutokuwa na kodi zisizokuwa na utulivu, lakini pia kuwa na sera ambazo zinabadilika badilika, hiki ni kitu ambacho hakivutii wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna watu wamewekeza kwenye elimu, uwekezaji kwenye elimu ni investment ya muda mrefu, return yake on investment ni zaidi ya miaka 10. Leo land rent unapokwenda kumchaji mtu mwenye shule binafsi, kwenye eneo la eka tatu katikati ya mji kwa mwaka anatakiwa kulipa milioni tisa, milioni sita inatoka wapi? Sasa uwekezaji umeanza kuwa kwa sababu hizi shule binafsi ndani ya manispaa lazima awe na eka tatu ndani yake kuna choo, viwanja vya michezo, madarasa, maabara, library vyote hadi choo kinachajiwa land rent, leo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inakuwaje wakati hawa watu binafsi ni wawekezaji, wametupunguzia msongamano kwenye shule zetu za public; lakini hawa watoto ni watoto wa Watanzania, Watanzania hawa wanaosomesha kwenye shule binafsi wana haki kabisa ya kuhudumiwa kielimu na Serikali hii, lakini wameamua kulipa kodi, wameendelea kusomesha watoto wao kwa gharama zingine, kwa nini tuwaongezee mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie katika hizi shule binafsi, Serikali inatumia zaidi ya gharama za asilimia 97 kumsomesha mtoto kwenye shule ya public, lakini haichangii chochote kwenye shule ya private. Leo hii shule ya private inalipia fire, yaani shule ikitaka kuungua lazima ilipe ili ije izimiwe moto. Leo hatuna hata grant ya temptation tunayopata, unalipa land rent wakati fulani Katibu wa Wizara ya Fedha aliona kwamba suala la kuchaji kodi kwenye shule wakati ni taasisi zinazotoa huduma akazuia tukatolewa kodi ya SDL; lakini kodi hii imerudishwa kwa mtindo wa ardhi.

Mheshimiwa Spika, vile vitu alivyoongea mama Samia kuangalia sera na kanuni zetu; kanuni mojawapo inayowatesa wananchi wa Tanzania ni ile kumpa commissioner room na kumpa power zaidi ya Bunge, nasema zaidi ya Bunge kwa sababu gani haiwezekani kwenye hati mtu aandikiwe hati hii utalipa kwa mwaka Sh.1,000,000 labda ndiyo itakuwa land rent yako; Kamishna anakaa anabadilisha mtu alipe milioni sita au milioni tisa nani hapo mwenye mamlaka kuu? Hivi ndivyo vipengele ambavyo Rais alisema viondolewe kwenye kanuni, sera zetu na sheria kama zinawakandamiza Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani leo tukafikiri viwanja vya michezo navyo vilipiwe kwa utaratibu upi? Tuwaangalie hawa watu kwa sababu ni wawekezaji wa ndani na tuwasaidie; na kwenye maeneo ya Makanisa, maeneo ya Vyuo, hawa wamechukua jukumu la Serikali la kuelimisha Watanzania, kwa nini tusiwasaidie kama hatusaidii hata kulipa mishahara, watu hawa hata fedha ya kukaguliwa, kuletewa mitihani, wanalipa mitihani, kukaguliwa lakini hawajalalamika. Unaposema watu hawa wanachaji fedha, basi umchaji kodi, ujue ile kodi inapelekwa moja moja kwa Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunawaomba ndugu zetu wa ardhi, kwa sababu wao ni msingi mmojawapo wa maendeleo kwa hiyo wasiposimamia vizuri sera hii na wakaweka kodi za aina hii maana yake ni kwamba huo mhimili hautasimama vizuri na hatutaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Ameshamaliza muda wake; ahsante sana Mheshimiwa Jesca.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nakushukuru sana. Naomba hilo lishughulikiwe.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi nikushukuru kwa ajili ya kunipa nafasi hii, lakini pia na mimi nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuona umuhimu wa kuanzisha Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii, lakini pia nimpongeze Waziri pamoja na wenzie wote kwa kazi kubwa ambayo wameanza kuifanya kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, mimi leo naomba niongelee watoto wa kiume; tangu uumbaji Mungu alivyoumba utaratibu kila kitu kina namna ya kuongezeka na katika baraka ambazo Mwenyezi Mungu alizitoa kwa viumbe alivyoviumba tukiwepo wanadamu alisema tukaongezeka, tukatiishe, tukazalishe na tukatawale, hivi ni vitu ambavyo Mwenyezi Mungu, lakini sasa tunakwenda kuongelea pale kwenye kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa wanadamu au mbegu ya wanadamu Mwenyezi Mungu ameiweka ndani ya mtoto wa kiume, hakuna namna utabisha hilo. Na hata katika wanyama mbegu yao ya kuongezeka ipo ndani ya yule mnyama wa kiume, kwenye samaki hivyo hivyo yaani kwenye viumbe vyote ni hivyo. Sasa watu wote wenye afya nzuri ya akili wanaitunza mbegu kuliko kituo chochote, mkulima yeyote mwenye busara anaitunza mbegu yake vizuri kuliko kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ndio maana mimi siwezi kuwa mshabiki wa kwamba mwanaume akifanya kosa ahasiwe kwa sababu mwisho Watanzania tutakosa mbegu na tukikosa mbegu tukaenda kuagiza kutoka nje sio Watanzania; na tukiitwa mbinguni kule tutaonekana Taifa letu liliisha siku nyingi sisi ni Taifa lingine. Sasa ninachotaka kusema, namna ambavyo tunaangalia watoto wetu wa kiume nchi hii sio sawa, naomba Mheshimiwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii alichukue ile ni mbegu, tukianza kwenye level ya familia tuangalie namna tunavyowalea watoto wetu wa kiume. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbegu unajua inaweka kwenye kihenge inatunzwa vizuri isibunguliwe, lakini leo kwenye level ya familia ukiangalia mtoto wa kike ameweka karibu kabisa na chumba cha baba na mama ili hata akitoka usiku washtuke wamlinde, mtoto wa kiume amewekewa chumba banda la uani huko, arudi hakurudi hakuna anayejua. Leo hii kwenye familia tunasema kwamba hawa ndio vichwa vya familia, lakini ukiangalia namna tunavyowalea sio kuja kuwa vichwa, ndio maana kunatokea mgongano sasa hivi, huwezi kutegemea kumlea mfalme halafu ukamlea kilezilezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tuangalie wengi hapa tunaweza tukawa tunaangalia kwenye Azam pale sinema ya Ertugul angalia Ertugul jinsi alivyo m-raise Ottoman, alivyompeleka vitani, alivyomsimulia kwamba wewe ni mfalme, alivyomfundisha na kumpa mbinu, alivyomlisha, alivyompeleka shule na kumpa maarifa ya kwamba yeye ni mfalme, lakini sivyo tunavyowalea watoto wetu wa kiume. Leo hii tunaanza kuwapa sifa za ufalme kabla hajafika kwenye kuwa mfalme, mtoto wa kiume anapendelewa, anapewa vitu hata akiumia tu wakati mwingine anahitaji faraja alie, amwambie mama mimi nimefanyiwa kitu kibaya leo watoto wetu wanalawitiwa kwenye majumba kwa sababu ameshaambiwa mtoto wa kiume halii lii, mtoto wa kiume hasemi semi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo anasindwa hata kujieleza tatizo lake, leo hii ukienda mitaani waliojaa ni watoto wa kiume, sio wa kike, wameachwa, leo hii tukienda kwenye elimu tukianza kuweka kipaumbele hapa tunaweka kipaumbele cha kujenga hostels tunajenga za wanawake sio za watoto wa kiume. Sisi tunaangalia equality hatuangalii equity, sasa huyu unayetegemea aje kuwa kichwa leo hii twende kwenye style tunavyowaozesha watoto wetu, watoto wa kike wanaitwa wanapewa kitchen party wanapewa mafunzo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa MzungumzajI

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema lazima sasa tubadilishe style ya kuangaia watoto wetu wa kiume na kuwapa haki sawa kwenye elimu, kwenye matibabu kwenye mafunzo kwenye kila kitu ili tuanze kuwa na kichwa kilichoenda shule, kama tunajua ile ndio mbegu yetu lazima tuitunze kwa ubora wote bila kuangalia kwamba …

SPIKA: Haya ahsante sana.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: … hawa ni watu wa aina gani, ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)