Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Lucy John Sabu (5 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuunga hoja iliyoko mezani. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunijalia kibali kuwa mahali hapa. Lakini nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuniamini hususani Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiupekee sana Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Simiyu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba ya Rais imeeleza mambo mengi ambayo yametoa dira na vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imewapa Tanzania matumaini makubwa hususan kwenye sekta mbalimbali za kiuchumi. Mambo haya yote yatafanikiwa endapo sisi tulioaminiwa kuwa wawakilishi wa wananchi wenzetu tutafanya kazi kwa bidii katika kumsaidia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijikite zaidi katika hotuba ya Mheshimiwa Rais hususan kwenye suala zima la mikopo itolewayo na Halmashauri zetu. Mikopo hii lengo la Serikali kuwaweza vijana lilikuwa ni nzuri zaidi endapo kama tutaendelea kuwajengea vijana uwezo hususan kwa kutoa elimu ya kutosha, lakini na mafunzo ya ujasiriamali. Kwa sababu kitu kinachotokea vijana wanapounda makundi wanakuwa hawana uzoefu na elimu ya kutosha hususan kwenye ujasiriamali wanakuwa hawana. Hivyo basi kama ambavyo tulivyo na miradi ya maendeleo ya kimkakati basi tulibebe na hili liwe ni fursa ya kimkakati hususan katika kuwaajiri vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kuishauri Serikali hususan kwenye hii mikopo isiwe ni sehemu muafaka sasa tuunde benki kwa ajili ya vijana ambapo hela zote ambazo zinatoka kwenye halmashauri ziingie kwenye ile benki ambayo tutaifungua lakini pia na mifuko hii ya uwezeshaji mifuko 18 ambayo ipo kwenye Ofisi ya Waziri iingie kwenye benki ambayo tutaianzisha. Nina imani kupitia kuanzisha benki hii itaweza kutoa mikopo kwa mtu mmoja tofauti na ambavyo inatolewa mikopo kwa vikundi. Kwa sababu kwenye vikundi kila mtu ana idea zake tofauti tofauti, unajikuta vijana hao wanashindwa kurudisha marejesho ya pesa wanazopewa Halmashauri zetu. Mwisho wa siku tunakuwa tunapoteza fedha ambazo zinakuwa ni changamoto kwenye Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano na ya Sita kwa kazi nzuri katika Mpango wa Pili wa kuimarisha uchumi wa viwanda ambapo viwanda vingi vimejengwa kati ya mwaka 2015 - 2020 vikiwemo viwanda vidogo, vya kati na vikubwa. Tuna imani kwa dhamira ya Rais wetu wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kazi iendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kubwa ataendelea kuweka mkazo mkubwa kwenye ujenzi wa viwanda hasa viwanda vinavyotumia malighafi zinazopatikana nchini Tanzania. Tunaunga mkono viwanda kwa sababu vinasaidia kuongeza thamani ya mazao yanayopatikana hapa nchini mfano; pamba, alizeti, katani na kadhalika, lakini pia kuboresha bei ya mazao kwa wakulima, kwani inaondoa gharama za usafirishaji kwenda nje ya nchi ambapo fedha inakwenda kumlipa mkulima, lakini pia ajira za wananchi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo nina mambo machache ya kuishauri Serikali, Simiyu ni mkoa unaoongoza kwa kilimo cha pamba, kutokana na ubunifu wa viongozi wa Simiyu, wakiongozwa na Mheshimiwa Anthony Mtaka na wasaidizi wake waliweza kubuni na kuishawishi Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, NHIF, WCF pamoja na Benki ya Uwezeshaji (TIB), TBS, TIRDO, TMDA kuanzishwa kwa kiwanda cha vifaatiba vitokanavyo na pamba; zaidi ya bidhaa 19 vikiwemo taulo za kike. Mkoa na Wilaya ya Bariadi ilitoa eneo lililoko kwenye maeneo yanayofikika na miundombinu ya maji, umeme, mawasiliano na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iliunda kampuni na Bodi ya Wakurugenzi, Serikali iliteua wataalamu waanzilishi wa kiwanda hicho na Serikali iligharamia safari za wataalamu kwenda nje kujifunza teknolojia stahiki kwa ajili ya kiwanda hicho na upembuzi yakinifu ulishafanyika, na gharama zote zilizokwisha kutumika ni shilingi milioni 915.98. Michakato yote ilianza toka mwaka 2016/2017 mpaka sasa hamna kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa mkoa wa Simiyu tungependa kufahamu maelezo ya kina kwa nini kiwanda hicho na ujenzi wake haujaanza?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajielekeza katika eneo la uwezeshaji wananchi kiuchumi, kwanza niipongeze Serikali kwa kuendelea kuratibu programu ya kuongeza ujuzi kitaifa kwa vijana ambayo imekuwa na tija kwa vijana wengi na wananufaika na fursa hizo.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa tuliyonayo ni vijana hawa wakishahitimu masomo yao, kujiajiri au kuajiriwa; natambua juhudi za Serikali kwamba baadhi ya wahitimu wamekuwa wakitafutiwa na kuunganishwa na waajiri wao lakini bado kuna vijana wengi hawajaweza kupata ajira au kuajiriwa kutokana na changamoto ya mtaji.

Mheshimiwa Spika, katika mkutano wa vijana Mwanza na Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alituarifu kuwa wataunda benki ya vijana wajasiriamali hapa nchini ili kutatua tatizo la mtaji kwa vijana, na ningeomba kuishauri Serikali; benki hiyo tunaomba izingatie vigezo na masharti vya nafasi ya vijana ambao wengi hawana dhamana ya kukopa, tunaiomba sana Serikali izingatie nafasi ya uchumi wa vijana wengi ambao hawana kazi rasmi na iweze kuwasaidia kupitia mawazo yao ya biashara, matamanio ya vijana wengi ni kuona benki hii inakuwa suluhisho la mtaji kwa vijana wengi.

Mheshimiwa Spika, sasa ningependa mtoa hoja wakati anahitimisha hoja yake atueleze mchakato wa kuunda benki ya vijana wajasiriamali umefikia wapi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja iliyopo mezani. Nami nitajikita katika uwezeshaji wa wananchi kiuchumi hususan katika ujuzi kwa vijana na ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa juhudi mbalimbali ambazo imekuwa ikizifanya hususan kwa vijana kupitia Programu ya Kukuza Ujuzi Kitaifa. Kupitia programu hii, nafahamu kwamba Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kukuza ujuzi kwa vijana na ili waweze kujiajiri na kuajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikiri kuwa mnufaika wa vijana hawa ambao wamekuwa wakipatiwa ujuzi kupitia vyuo vya VETA hususan kwenye kurasimisha ujuzi lakini pia VETA wamekuwa ni watu ambao wanawasaidia vijana hawa kuwashikiza hususan kwa waajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vijana hawa kupatiwa ujuzi na kujiajiri ni vitu viwili tofauti. Nikichukulia mfano, tulipokuwa na ziara ya Kamati tulitembelea TIRDO (Tanzania Industrial Research and Development Organization) ambapo tulikutana na vijana ambao wana ujuzi ama ubunifu wameweza kutengeneza taa ambapo zina uwezo hata kama ukiwa nje ya nyumba yako, wame-install program kwenye simu ukai-request kwamba zima ama washa taa hata kama ukiwa nje ya nchi. Changamoto inakuja kumekuwa na vijana wengi ambao wana ujuzi wa aina mbalimbali lakini wanashindwa kujiajiri kwa kukosa mtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi napenda kuiomba Serikali yangu na kuishauri kwa kuwa tuna Programu ya Kukuza Ujuzi kwa Vijana ije na utaratibu wa kutengeneza fursa za kimkakati. Kwa mfano, tunao vijana ambao wana ujuzi wa ufundi seremala na kuna baadhi ya maeneo ambayo yana upungufu wa madawati, Serikali inaweza ikatengeneza fursa kwa vijana hawa wenye ufundi wa useremala kwa kutengeneza kambi rasmi na kuweza kuchukua vijana hawa kuwapa tender ya kutengeneza madawati kwa kuwapa materials na vitendea kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu Serikali imekuwa ikitoa mikopo kwa ajili ya vijana hususan kwenye Halmashauri zetu. Tunaishukuru Serikali yetu Sikivu, kipindi cha nyuma tulipiga kelele sana Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu makundi yalikuwa yakiundwa na watu kumi kumi lakini tarehe 26 Februari, kupitia Ofisi ya Wizara ya TAMISEMI ililegeza masharti ya mikopo na kuboresha zaidi kutoa nafasi kwamba hata wakiwa vijana watano wana uwezo wa kukopa mkopo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini matamanio ya vijana wenzetu ni kuwa mkopo huu uwe ni wa mtu mmoja mmoja. Kama Serikali imeweza kutoa mikopo kwa mtu mmoja mmoja hususan kwenye mikopo ya vyuo vikuu, naomba na hili Serikali ilifanyie kazi. Hii ni kwa sababu mikopo ya watu kwenye makundi inakuwa ina mambo mengi, kila mtu anakuwa ana interest zake kwenye ideas ambayo wanafanya kwenye biashara husika. Niiombe sana Serikali yetu sikivu iweze kutusaidia kwenye jambo hili ili liweze kuwa la manufaa zaidi kwa vijana wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote, niiombe Serikali yetu iendelee kutoa elimu kwa vijana wote ambao wanachukua mikopo kwenye Halmashauri. Nasema hivi kwa sababu vijana wanakuwa na interest tofauti tofauti, hivyo, mkopo unavyochukuliwa bila elimu ya kutosha matumizi yanakuwa tofauti na marejesho yanashindwa kufikiwa kwa wakati muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja iliyopo mezani. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii nami niweze kuchangia hoja iliyoko Mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri ambayo inafanya. Nitumie fursa hii pia kuzipongeza Wizara zote mbili; ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara pamoja na Wizara ya Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa niende moja kwa moja kwenye hoja, na ninapenda kuchangia katika Shirika letu la SIDO. Kwanza kabisa kama ambavyo sote tunafahamu kwamba shirika hili lilianzishwa mahususi kwa kuwezesha viwanda vidogovidogo pamoja na kuongeza rasilimali katika bidhaa zetu na kutumia teknolojia mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu, tumekuwa na ubunifu mwingi na vijana wengi wamekuwa ni wabunifu. Na kama Kamati tulipata fursa ya kutembelea TIRDO na pale tuliona kuna vijana wengi ambao wamekuwa wakibuni teknolojia mbalimbali. Mfano, tuliona kuna vijana ambao wamebuni application ya taa ambapo kupitia application hiyo unaweza ukawasha taa ukiwa ndani ama nje ama umbali mrefu lakini changamoto kubwa ya uendelezaji wa ubunifu huu ni kwamba vijana wengi hawana mtaji wa kuendeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Kamati, na mtaona hata kwenye taarifa yetu, tumeomba ama tumeshauri Serikali kuona uwezekano kupitia SIDO na wataalam wake waone namna ya kubuni vyanzo mbadala ambavyo wanaweza wakawasaidia vijana hawa ili waweze kuendeleza ubunifu wao. Lakini pamoja na hayo, Serikali ione namna ya kuandika maandiko mbalimbali kupitia miradi mbalimbali ambayo itawasaidia wao waweze kupata zile fedha zilizopo katika Global Innovation Fund kupitia washirika mbalimbali wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, Serikali iweze kuona vijana hawa wanaendeleza ubunifu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua jitihada za Serikali katika kuhakikisha kwamba vijana wanajiajiri. Na katika eneo hili upande wa SIDO tunatambua kwamba kuna mikopo midogomidogo inatolewa kupitia Mfuko wa Uwezeshaji wa NEDF na tunaona juhudi hizo kupitia kwamba wanatoa mikopo yenye riba ya asilimia tisa upande wa miradi ya uzalishaji na asilimia 12 upande wa miradi ya kibiashara. Na kiwango kikubwa ambacho wanatoa ni kiasi cha shilingi milioni tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninapenda kuishauri Serikali kwa mjasiriamali ambaye anaanzisha kiwanda kidogo, milioni tano bado ni ndogo. Na kama mnavyofahamu, kiwanda au kubuni teknolojia kunahitaji kiwango kikubwa cha fedha. Sasa milioni tano bado ni kiwango kidogo. Niiombe Serikali iongeze kiwango hiki walau ikiwa kama milioni kumi itaweza kuwasaidia wajasiriamali wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la kuwezesha bidhaa za wajasiriamali hawa kufikia masoko. Tunatambua kwamba Serikali imekuwa ikitoa mafunzo lakini bado kuna changamoto upande wa wajasiriamali wetu; wanahitaji elimu zaidi upande wa branding, labelling na packaging ya bidhaa zao ili ziweze kushindana na bidhaa zinazoenda nje. Sasa TBS wanalo jukumu la msingi kuhakikisha kwamba bidhaa za wajasiriamali wetu zinathibitishwa ili ziweze kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama ambavyo tunafahamu online businesses (masoko ya kimtandao), watu wengi katika kipindi hiki wamekuwa wakitumia masoko ya kimtandao. Sasa upande wa SIDO nilikuwa nikiangalia hapa utendaji wao wa kazi upande wa digital marketing bado ni mdogo kwa sababu bado watu hawajawa na uelewa mpana kuhusiana na shughuli ambazo zinafanywa na SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nimeangalia upande wa Instagram kwenye page yao wana 35.8k followers na upande wa Facebook wana 8k followers. Bado hawajajitangaza vya kutosha. Kwa hiyo, ninapenda kushauri watumie mitandao ili waweze kufikia idadi kubwa ya watu na waweze kujua vitu ambavyo vinafanywa na SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ninapenda kuzungumza; EPZA walitwaa maeneo ya wananchi upande wa Bagamoyo na Bunda, yalitwaliwa kwa ajili ya kuendeleza viwanda na sasa imekuwa muda mrefu maeneo hayo bado wananchi hawajalipwa fidia. Kwa hiyo, ninapenda kuishauri Serikali, na kupitia Kamati yetu tumeiomba, kwamba wananchi hawa walipwe fidia zao ili fedha watakazopata ziweze kuwasaidia kuendeleza maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii. Ahsante. (Makofi)