Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Lucy John Sabu (10 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuunga hoja iliyoko mezani. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunijalia kibali kuwa mahali hapa. Lakini nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kuniamini hususani Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiupekee sana Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Simiyu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba ya Rais imeeleza mambo mengi ambayo yametoa dira na vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imewapa Tanzania matumaini makubwa hususan kwenye sekta mbalimbali za kiuchumi. Mambo haya yote yatafanikiwa endapo sisi tulioaminiwa kuwa wawakilishi wa wananchi wenzetu tutafanya kazi kwa bidii katika kumsaidia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijikite zaidi katika hotuba ya Mheshimiwa Rais hususan kwenye suala zima la mikopo itolewayo na Halmashauri zetu. Mikopo hii lengo la Serikali kuwaweza vijana lilikuwa ni nzuri zaidi endapo kama tutaendelea kuwajengea vijana uwezo hususan kwa kutoa elimu ya kutosha, lakini na mafunzo ya ujasiriamali. Kwa sababu kitu kinachotokea vijana wanapounda makundi wanakuwa hawana uzoefu na elimu ya kutosha hususan kwenye ujasiriamali wanakuwa hawana. Hivyo basi kama ambavyo tulivyo na miradi ya maendeleo ya kimkakati basi tulibebe na hili liwe ni fursa ya kimkakati hususan katika kuwaajiri vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa kuishauri Serikali hususan kwenye hii mikopo isiwe ni sehemu muafaka sasa tuunde benki kwa ajili ya vijana ambapo hela zote ambazo zinatoka kwenye halmashauri ziingie kwenye ile benki ambayo tutaifungua lakini pia na mifuko hii ya uwezeshaji mifuko 18 ambayo ipo kwenye Ofisi ya Waziri iingie kwenye benki ambayo tutaianzisha. Nina imani kupitia kuanzisha benki hii itaweza kutoa mikopo kwa mtu mmoja tofauti na ambavyo inatolewa mikopo kwa vikundi. Kwa sababu kwenye vikundi kila mtu ana idea zake tofauti tofauti, unajikuta vijana hao wanashindwa kurudisha marejesho ya pesa wanazopewa Halmashauri zetu. Mwisho wa siku tunakuwa tunapoteza fedha ambazo zinakuwa ni changamoto kwenye Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano na ya Sita kwa kazi nzuri katika Mpango wa Pili wa kuimarisha uchumi wa viwanda ambapo viwanda vingi vimejengwa kati ya mwaka 2015 - 2020 vikiwemo viwanda vidogo, vya kati na vikubwa. Tuna imani kwa dhamira ya Rais wetu wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kazi iendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kubwa ataendelea kuweka mkazo mkubwa kwenye ujenzi wa viwanda hasa viwanda vinavyotumia malighafi zinazopatikana nchini Tanzania. Tunaunga mkono viwanda kwa sababu vinasaidia kuongeza thamani ya mazao yanayopatikana hapa nchini mfano; pamba, alizeti, katani na kadhalika, lakini pia kuboresha bei ya mazao kwa wakulima, kwani inaondoa gharama za usafirishaji kwenda nje ya nchi ambapo fedha inakwenda kumlipa mkulima, lakini pia ajira za wananchi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo nina mambo machache ya kuishauri Serikali, Simiyu ni mkoa unaoongoza kwa kilimo cha pamba, kutokana na ubunifu wa viongozi wa Simiyu, wakiongozwa na Mheshimiwa Anthony Mtaka na wasaidizi wake waliweza kubuni na kuishawishi Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, NHIF, WCF pamoja na Benki ya Uwezeshaji (TIB), TBS, TIRDO, TMDA kuanzishwa kwa kiwanda cha vifaatiba vitokanavyo na pamba; zaidi ya bidhaa 19 vikiwemo taulo za kike. Mkoa na Wilaya ya Bariadi ilitoa eneo lililoko kwenye maeneo yanayofikika na miundombinu ya maji, umeme, mawasiliano na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iliunda kampuni na Bodi ya Wakurugenzi, Serikali iliteua wataalamu waanzilishi wa kiwanda hicho na Serikali iligharamia safari za wataalamu kwenda nje kujifunza teknolojia stahiki kwa ajili ya kiwanda hicho na upembuzi yakinifu ulishafanyika, na gharama zote zilizokwisha kutumika ni shilingi milioni 915.98. Michakato yote ilianza toka mwaka 2016/2017 mpaka sasa hamna kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa mkoa wa Simiyu tungependa kufahamu maelezo ya kina kwa nini kiwanda hicho na ujenzi wake haujaanza?
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajielekeza katika eneo la uwezeshaji wananchi kiuchumi, kwanza niipongeze Serikali kwa kuendelea kuratibu programu ya kuongeza ujuzi kitaifa kwa vijana ambayo imekuwa na tija kwa vijana wengi na wananufaika na fursa hizo.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa tuliyonayo ni vijana hawa wakishahitimu masomo yao, kujiajiri au kuajiriwa; natambua juhudi za Serikali kwamba baadhi ya wahitimu wamekuwa wakitafutiwa na kuunganishwa na waajiri wao lakini bado kuna vijana wengi hawajaweza kupata ajira au kuajiriwa kutokana na changamoto ya mtaji.

Mheshimiwa Spika, katika mkutano wa vijana Mwanza na Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alituarifu kuwa wataunda benki ya vijana wajasiriamali hapa nchini ili kutatua tatizo la mtaji kwa vijana, na ningeomba kuishauri Serikali; benki hiyo tunaomba izingatie vigezo na masharti vya nafasi ya vijana ambao wengi hawana dhamana ya kukopa, tunaiomba sana Serikali izingatie nafasi ya uchumi wa vijana wengi ambao hawana kazi rasmi na iweze kuwasaidia kupitia mawazo yao ya biashara, matamanio ya vijana wengi ni kuona benki hii inakuwa suluhisho la mtaji kwa vijana wengi.

Mheshimiwa Spika, sasa ningependa mtoa hoja wakati anahitimisha hoja yake atueleze mchakato wa kuunda benki ya vijana wajasiriamali umefikia wapi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja iliyopo mezani. Nami nitajikita katika uwezeshaji wa wananchi kiuchumi hususan katika ujuzi kwa vijana na ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa juhudi mbalimbali ambazo imekuwa ikizifanya hususan kwa vijana kupitia Programu ya Kukuza Ujuzi Kitaifa. Kupitia programu hii, nafahamu kwamba Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kukuza ujuzi kwa vijana na ili waweze kujiajiri na kuajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikiri kuwa mnufaika wa vijana hawa ambao wamekuwa wakipatiwa ujuzi kupitia vyuo vya VETA hususan kwenye kurasimisha ujuzi lakini pia VETA wamekuwa ni watu ambao wanawasaidia vijana hawa kuwashikiza hususan kwa waajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vijana hawa kupatiwa ujuzi na kujiajiri ni vitu viwili tofauti. Nikichukulia mfano, tulipokuwa na ziara ya Kamati tulitembelea TIRDO (Tanzania Industrial Research and Development Organization) ambapo tulikutana na vijana ambao wana ujuzi ama ubunifu wameweza kutengeneza taa ambapo zina uwezo hata kama ukiwa nje ya nyumba yako, wame-install program kwenye simu ukai-request kwamba zima ama washa taa hata kama ukiwa nje ya nchi. Changamoto inakuja kumekuwa na vijana wengi ambao wana ujuzi wa aina mbalimbali lakini wanashindwa kujiajiri kwa kukosa mtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi napenda kuiomba Serikali yangu na kuishauri kwa kuwa tuna Programu ya Kukuza Ujuzi kwa Vijana ije na utaratibu wa kutengeneza fursa za kimkakati. Kwa mfano, tunao vijana ambao wana ujuzi wa ufundi seremala na kuna baadhi ya maeneo ambayo yana upungufu wa madawati, Serikali inaweza ikatengeneza fursa kwa vijana hawa wenye ufundi wa useremala kwa kutengeneza kambi rasmi na kuweza kuchukua vijana hawa kuwapa tender ya kutengeneza madawati kwa kuwapa materials na vitendea kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu Serikali imekuwa ikitoa mikopo kwa ajili ya vijana hususan kwenye Halmashauri zetu. Tunaishukuru Serikali yetu Sikivu, kipindi cha nyuma tulipiga kelele sana Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu makundi yalikuwa yakiundwa na watu kumi kumi lakini tarehe 26 Februari, kupitia Ofisi ya Wizara ya TAMISEMI ililegeza masharti ya mikopo na kuboresha zaidi kutoa nafasi kwamba hata wakiwa vijana watano wana uwezo wa kukopa mkopo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini matamanio ya vijana wenzetu ni kuwa mkopo huu uwe ni wa mtu mmoja mmoja. Kama Serikali imeweza kutoa mikopo kwa mtu mmoja mmoja hususan kwenye mikopo ya vyuo vikuu, naomba na hili Serikali ilifanyie kazi. Hii ni kwa sababu mikopo ya watu kwenye makundi inakuwa ina mambo mengi, kila mtu anakuwa ana interest zake kwenye ideas ambayo wanafanya kwenye biashara husika. Niiombe sana Serikali yetu sikivu iweze kutusaidia kwenye jambo hili ili liweze kuwa la manufaa zaidi kwa vijana wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote, niiombe Serikali yetu iendelee kutoa elimu kwa vijana wote ambao wanachukua mikopo kwenye Halmashauri. Nasema hivi kwa sababu vijana wanakuwa na interest tofauti tofauti, hivyo, mkopo unavyochukuliwa bila elimu ya kutosha matumizi yanakuwa tofauti na marejesho yanashindwa kufikiwa kwa wakati muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja iliyopo mezani. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii nami niweze kuchangia hoja iliyoko Mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri ambayo inafanya. Nitumie fursa hii pia kuzipongeza Wizara zote mbili; ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara pamoja na Wizara ya Mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa niende moja kwa moja kwenye hoja, na ninapenda kuchangia katika Shirika letu la SIDO. Kwanza kabisa kama ambavyo sote tunafahamu kwamba shirika hili lilianzishwa mahususi kwa kuwezesha viwanda vidogovidogo pamoja na kuongeza rasilimali katika bidhaa zetu na kutumia teknolojia mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu, tumekuwa na ubunifu mwingi na vijana wengi wamekuwa ni wabunifu. Na kama Kamati tulipata fursa ya kutembelea TIRDO na pale tuliona kuna vijana wengi ambao wamekuwa wakibuni teknolojia mbalimbali. Mfano, tuliona kuna vijana ambao wamebuni application ya taa ambapo kupitia application hiyo unaweza ukawasha taa ukiwa ndani ama nje ama umbali mrefu lakini changamoto kubwa ya uendelezaji wa ubunifu huu ni kwamba vijana wengi hawana mtaji wa kuendeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Kamati, na mtaona hata kwenye taarifa yetu, tumeomba ama tumeshauri Serikali kuona uwezekano kupitia SIDO na wataalam wake waone namna ya kubuni vyanzo mbadala ambavyo wanaweza wakawasaidia vijana hawa ili waweze kuendeleza ubunifu wao. Lakini pamoja na hayo, Serikali ione namna ya kuandika maandiko mbalimbali kupitia miradi mbalimbali ambayo itawasaidia wao waweze kupata zile fedha zilizopo katika Global Innovation Fund kupitia washirika mbalimbali wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, Serikali iweze kuona vijana hawa wanaendeleza ubunifu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua jitihada za Serikali katika kuhakikisha kwamba vijana wanajiajiri. Na katika eneo hili upande wa SIDO tunatambua kwamba kuna mikopo midogomidogo inatolewa kupitia Mfuko wa Uwezeshaji wa NEDF na tunaona juhudi hizo kupitia kwamba wanatoa mikopo yenye riba ya asilimia tisa upande wa miradi ya uzalishaji na asilimia 12 upande wa miradi ya kibiashara. Na kiwango kikubwa ambacho wanatoa ni kiasi cha shilingi milioni tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninapenda kuishauri Serikali kwa mjasiriamali ambaye anaanzisha kiwanda kidogo, milioni tano bado ni ndogo. Na kama mnavyofahamu, kiwanda au kubuni teknolojia kunahitaji kiwango kikubwa cha fedha. Sasa milioni tano bado ni kiwango kidogo. Niiombe Serikali iongeze kiwango hiki walau ikiwa kama milioni kumi itaweza kuwasaidia wajasiriamali wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la kuwezesha bidhaa za wajasiriamali hawa kufikia masoko. Tunatambua kwamba Serikali imekuwa ikitoa mafunzo lakini bado kuna changamoto upande wa wajasiriamali wetu; wanahitaji elimu zaidi upande wa branding, labelling na packaging ya bidhaa zao ili ziweze kushindana na bidhaa zinazoenda nje. Sasa TBS wanalo jukumu la msingi kuhakikisha kwamba bidhaa za wajasiriamali wetu zinathibitishwa ili ziweze kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama ambavyo tunafahamu online businesses (masoko ya kimtandao), watu wengi katika kipindi hiki wamekuwa wakitumia masoko ya kimtandao. Sasa upande wa SIDO nilikuwa nikiangalia hapa utendaji wao wa kazi upande wa digital marketing bado ni mdogo kwa sababu bado watu hawajawa na uelewa mpana kuhusiana na shughuli ambazo zinafanywa na SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nimeangalia upande wa Instagram kwenye page yao wana 35.8k followers na upande wa Facebook wana 8k followers. Bado hawajajitangaza vya kutosha. Kwa hiyo, ninapenda kushauri watumie mitandao ili waweze kufikia idadi kubwa ya watu na waweze kujua vitu ambavyo vinafanywa na SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ninapenda kuzungumza; EPZA walitwaa maeneo ya wananchi upande wa Bagamoyo na Bunda, yalitwaliwa kwa ajili ya kuendeleza viwanda na sasa imekuwa muda mrefu maeneo hayo bado wananchi hawajalipwa fidia. Kwa hiyo, ninapenda kuishauri Serikali, na kupitia Kamati yetu tumeiomba, kwamba wananchi hawa walipwe fidia zao ili fedha watakazopata ziweze kuwasaidia kuendeleza maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii ili niweze kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuwaletea maendeleo wananchi. Kiupekee nimpongeze kwa kutoa pikipiki 7,000 na vitendea kazi kwa Maafisa Ugani, nina imani itawezesha kufanya kazi kwa weledi mkubwa na kuweza kuwafikia wakulima na kutatua changamoto zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020 imeahidi ajira zisizopungua 8,000,000 na tunatambua sote changamoto ya ajira iliyopo kwa vijana. Nimepitia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo, nimefarijika zaidi nilipoona vijana tumeguswa kupitia bajeti hii. Nichukue nafasi hii kuwapongeza Wizara ya Kilimo, kiupekee kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Hussein Bashe; Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara. Nina imani kupitia mradi huu ambao unaenda kuanzishwa hususan kwa vijana tutaweza kunufaika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze, kupitia bajeti tumeona kuna mradi unaenda kuanzishwa unaitwa Jenga Kesho Bora (Building a Better Tomorrow) Mradi mahususi kwa ajili ya vijana ambao wanaenda ku-fund, watatoa mtaji, watatota ardhi, watatoa mbegu, mafunzo, lakini pia watatafuta masoko kwa ajili ya bidhaa za mradi watakaouanzisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mradi huu, Mheshimiwa Waziri atakuwa shahidi wakati anautangaza kwenye mitandao ya kijamii, aliona namna gani vijana wengi wamevutiwa nao na wapo tayari kushiriki katika mradi huo. Nimefarijirika zaidi nimeona fedha imetengwa kiasi cha bilioni nne ambayo itakwenda kuwasaidia vijana hawa ili waweze kufanya mradi huu kwa ubunifu wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutoa ushauri wangu katika maeneo mawili hususan kwenye huu mradi. Nimeona mradi huu kwa majaribio utaanza Dodoma. Ningependa kushauri, Mheshimiwa Waziri tunaomba mradi huu usambae kwa nchi nzima ili vijana wengi waweze kunufaika. Pia tungependa kushauri hususan namna na utaratibu ambao utawekwa kwa ajili ya vijana au walengwa waweze kushiriki mradi huu, ningeshauri uwekwe utaratibu mzuri ambao vijana wengi waweze kuchaguliwa wale walengwa ambao kweli wanayo interest ya kufanya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii hususan kwa Mkoa wetu wa Simiyu nimpongeze Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa yeye ameshatoa mashamba na mwaka jana kuna vijana ambao walipewa mashamba na wameshaanza ninaomba tu Mheshimiwa Waziri ikikupendeza basi kwenye hiyo Bilioni Nne na Mkoa wa Simiyu uweze kutuona ili tuweze kunufaika na mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuwaomba, niliona mwaka huu kwa mara ya kwanza kuna vijana walipelekwa kwenye maonesho ya Dubai na Uturuki, ninawaomba Wizara waendelee na utaratibu huu wa kuwajengea uwezo lakini vijana wengi waweze kujifunza wenzetu huko nje wanafanya kilimo cha aina gani ili tuweze kunufaika lakini pia vijana wengi waweze kujiajiri katika sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa fursa hii ili nami niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Rais TAMISEMI. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuipongeza Wizara kwa uwasilishaji mzuri wa hotuba ya bajeti; lakini kwa namna ya pekee nimpongeze Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuleta maendeleo kwa wananchi. Sote ni mashuhuda, katika kipindi chake cha miaka hii miwili, tumejionea namna ambavyo anatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi; hususan katika eneo la elimu, sote ni mashuhuda shule nyingi zimejengwa, zaidi ya Shule 23,000. Pia ujenzi wa shule maalum za za bweni kwa wasichana kuanzia form one hadi form six. Pia vituo vya Afya vimejengwa katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa na mambo matatu. Jambo la kwanza ni kuhusiana na hili suala la mikopo ya asilimia kumi kwa wanawake, vijana na wenye ulemavu. Sote tulisikia hotuba aliyohitimisha jana Mheshimiwa Waziri Mkuu. Katika maelekezo ambayo aliyatoa ni kwamba usitishaji wa mikopo hiyo ni hadi hapo Serikali itakapojipanga na kuboresha mfumo wa utoaji wa mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, na mimi nikiwa kama mwakilishi wa vijana nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kuona jambo hili na umuhimu wake kwa sababu mikopo hii imekuwa ikitunufaisha kwa namna moja ama nyingine hususan kwa vijana ambao wanapomaliza vyuo wanakuwa hawana sehemu ya kuanzia. Hivyo basi mikopo hii imekuwa mkombozi mkubwa sana, na mimi naunga mkono maelekezo ambayo aliyatoa Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na maelekezo ambayo aliyatoa Mheshimiwa Rais. Kwamba ipo haja ya Serikali kuangalia namna ya kuingiza katika mfumo wa kibenki ili kuratibu suala zima la utoaji na urejeshaji wa mikopo.

Mheshimiwa Spika, sote tunatambua kwamba kumekuwa na vikundi hewa vikiendelea na wakati mwingine uwazi kwenye mikopo hii unakuwa hauonekani. Hivyo basi sisi kama vijana tunaunga mkono jambo hili na tuna imani kwamba Serikali inaenda kutengeneza mfumo ambao utasaidia vijana wengi waweze kunufaika. Hii ni kwa sababu kwenye mikopo iliyokuwa ikitolewa na wakati mwingine vikundi vinavyoundwa vijana wanakuwa hawana uelewa mzuri wa project ambayo wanaiendea; lakini na elimu ya biashara pia na upande wa ku-manage fedha ambazo wanafanya katika miradi yao. hivyo Serikali iweze kuangalia jambo hili kwa uzito mkubwa ili vijana wengi waweze kupata na mikopo hii iweze kuwa na tija. Hivyo basi kama itawezekana, kama wengine wataendelea na vikundi ama kutolewa mkopo wa mtu mmoja mmoja ili kila kijana kadri ambavyo atakuwa amejipanga aweze kuona anatumiaje fedha ambazo zinatolewa.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili ambalo ningependa kulizungumzia ni taulo za kike shuleni. Kwa muda sasa jambo hili limekuwa halina majawabu kwa sababu kama sote tunavyotambua tumefanya uboreshaji mkubwa katika eneo zima la elimu kwenye shule. Kwa namna ambavyo tunapambana katika kuboresha elimu lakini pia mtoto wa kike ni lazima aangaliwe kwa jicho la kitofauti kwa sababu mabinti wanapoingia katika siku zao wanapata changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, takwimu za UNICEF zinaonesha asilimia 10 ya watoto duniani wanakosa masomo kutokana na kipindi cha hedhi lakini pia wakiwa kwenye siku zao wanakosa kujiamini. Hivyo, tuiombe Serikali na nimefurahi nimeona upande wa maoni na ushauri wa Kamati wameongelea juu ya jambo hili. Hivyo basi. niiombe Serikali iweze kuona namna bora ya kuratibu jambo hili ili watoto au mabinti wa kike walioko mashuleni waweze kusaidiwa katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu natambua katika Serikali ya awamu ya nne ilitoa waraka ambao utatoa pad kwa watoto wa kike mashuleni, lakini waraka huu umekuwa hautekelezwi ipasavyo. Hivyo basi, niiombe Serikali iweze kutenga bajeti mahususi kwa ajili ya mbinti mashuleni ili waweze kuondokana na adha hii ambayo wanakumbana nayo.

Mheshimiwa Spika, nina imani hata tukianzisha viwanda vidogo vidogo kwenye halmashauri zetu ama kwenye ngazi za mkoa kwa ajili ya kutengeneza hizi taulo za kike, tutakuwa tumemlinda mtoto wa kike, lakini pia mtoto wa kike atasoma kwa kujiamini pasipokuwa na changamoto ama adha ya aina yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba sisi Wabunge tumekuwa tukipeleka pad mashuleni lakini pia kuna baadhi ya wadau mbalimbali wamekuwa waki-support jambo hili lakini bado uhitaji ni mkubwa. Kule vijijini uhitaji ni mkubwa sana kwa sababu baadhi ya watoto wamekuwa wanakata kanga, vitenge ama magazeti wakati mwingine na hii ni hatarishi kwa afya zao. Hivyo basi, tunaomba Wizara ya TAMISEMI waweze kuangalia jambo hili ili kumsaidia mtoto wa kike aweze kuondokana na changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, sisi Mkoa wa Simiyu ni kinara katika uzalishaji wa zao la pamba na kulikuwa na mpango wa Serikali wa kuanzisha kiwanda cha vifaatiba na moja ya malighafi ilikuwa ni kutumia pamba ikiwemo kuzalisha taulo za kike. Niombe basi kama jambo hili litakuwa gumu kutekelezwa kwenye halmashauri basi kwa kuwa sisi Mkoa wa Simiyu tunazalisha pamba kwa wingi waweze kutupa jukumu hili ili tutakapokuwa tunazalisha hizi taulo za kike ziweze kuwanufaisha nchi nzima. Vile vile TAMISEMI waweze kutusaidia ili kuharakisha jambo hili liweze kutekelezwa kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama MSD wameweza kutengeneza mipira ya wanaume na kugawa bure, iweje basi jambo hili lishindikane kutekelezwa kwa kutoa pads za watoto wa kike? Hivyo basi, niombe jambo hili waliangalie kwa jicho la kitofauti ili kuweza kumsaidia huyu mtoto wa kike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo ningependa kulizungumzia, kwenye halmashauri zetu kuna miradi ya kimkakati ambayo ilianzishwa kwa lengo la kuongeza mapato kwenye halmashauri, lakini pia kupunguza utegemezi katika bajeti ya Serikali Kuu. Katika Wilaya yetu ya Maswa, Mkoani Simiyu kuna Kiwanda cha Chaki kilianzishwa. Hivyo basi, niombe kwa sababu kulikuwa kuna fedha ambayo haijakamilika kutolewa kiasi cha Shilingi Bilioni mbili kwa ajili ya operating cost na umuhimu wa kiwanda hiki ni kutoa ajira kwa vijana 250, vile vile zitaweza kuzalishwa chaki ambazo zitasambazwa nchi nzima, niombe basi Serikali iweze kukamilisha jambo hili na fedha iweze kutolewa ili kiwanda hiki kiweze kuanza mara moja.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa fursa hii na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii nami niweze kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nachukua nafasi hii kumpongeza Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuleta maendeleo kwa wananchi. Nampongeza zaidi kupitia hizi fedha za mafunzo kwa vijana. Kwa kweli mama anafanya kazi kubwa katika kuhakikisha kwamba anatengeneza vijana matajiri katika sekta hii ya mifugo na uvuvi. Nadhani sote tunatambua kwamba, ni moja kati ya sekta ambayo wananchi wetu wengi wamejiajiri katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nichukue nafasi hii kuipongeza Wizara inayoongozwa na mtani wangu, Mheshimiwa Abdallah Ulega, pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa na mambo mawili ya kuzungumza. Jambo la kwanza ni vijana wanaopatiwa mafunzo ya unenepeshaji mifugo. Naunga mkono kupitia mzungumzaji aliyemaliza kuongea kwamba, ipo haja kubwa sana ya kuongezewa fedha kwenye huu mradi ili uweze kusambaa nchi nzima na uweze kuwanufaisha vijana wengi kupitia mradi huu. Ni mmoja wa miradi ambao una matokeo ya haraka kama ambavyo tumeona, unenepeshaji wa ng’ombe unahitaji miezi mitatu na ndani ya miezi mitatu unaweza kuuza ng’ombe kwa kuhakikisha kwamba tunapata fedha katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishauri Wizara kwamba vijana kama ambavyo tumeona wanahusishwa kwenye jambo hili la huu mradi wa unenepeshaji wa ng’ombe, ipo haja kubwa sana tuweze kuona uwazi wa vijana hawa ambao wanachaguliwa kwenda kwenye haya mafunzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye hotuba kwamba tuna vituo nane na viko katika mikoa mitatu; Tanga, Mwanza, na Kagera. Bado vituo hivi ni vichache na havijasambaa nchi nzima, na vijana wengi wanahamasika katika eneo hili ili waweze kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema, hadi kufikia Machi, 2023 vijana 238 wako kwenye huu mradi. Bado hii idadi ni ndogo sana, na kwa mwenendo huu, tija yake haiwezi ikaonekana kwa haraka. Hivyo basi, nashauri ushirikishwaji, ama waongeze idadi ya vijana wengi waweze kuwa-recruit kwenye huu mradi ili basi tuweze kuona tija yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema kwamba mnufaika atapewa ng’ombe 10 wa kunenepesha na kuwauza kila baada ya miezi mitatu, basi Wizara iongeze fedha za kutosha ili basi vijana wengi waweze kuhusishwa katika mradi huu. Nashauri Waziri wa fedha aongeze fedha katika mradi huu uweze kuinua vipato vya vijana wengi na kukuza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo kwenye ufugaji wa vizimba, tunampongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekuwa akizungumzia mara kwa mara juu ya mradi huu, mradi ambao utawanufaisha vijana wengi. Nasisitiza zaidi kwamba Wizara iweke mpango mzuri ambao utawasaidia vijana wengi waweze kujiajiri katika eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo napenda kuzungumzia ni zoezi la utambuzi na ufuatiliaji wa mifugo. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake, ukurasa wa 27, nanukuu: “Aidha tarehe 3 Novemba, 2022 Serikali ilisitisha zoezi la utambuzi wa mifugo kwa muda ili kurekebisha kasoro zilizojitokeza hapo awali.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri hajatupatia way forward, baada ya haya yote, nini changamoto waliyoiona? Wamejipangaje hususan katika ku-resume jambo hili ili liweze kufanukiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kwamba ni takwa la kisheria kuweza kupitia Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Mifugo ya Mwaka 2006 na Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba jambo hili ni muhimu ili tuweze kuwa na taarifa sahihi ya mifugo katika maeneo yetu. Pia, Serikali iweze kuboresha sera ama kuweza kuwa na idadi kamili ya mifugo tuliyonayo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba, zoezi hili lilikuwa lina changamoto mbalimbali kama malalamiko katika ada, upungufu wa kanuni, usimamizi, na utekelezaji wake. Sasa tungependa kufahamu ama kusikia wakati Mheshimiwa Waziri anahitimisha hoja yake tuweze kujua wamejipangaje katika zoezi hili ili kusaidia wafugaji wetu? Ama Serikali yetu kumsaidia mfugaji na kuboresha miundombinu ya wafugaji wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi la kuhesabu mifugo ni muhimu sana. Baadhi ya wananzengo ama wananchi, wamekuwa wakilitafakari na wakihoji kwamba mwaka 2022 tumetumia zaidi ya Shilingi bilioni 200 katika zoezi la sensa, na zoezi hili lilifanikiwa kwa asilimia 100. Sasa kwa mwananzengo wa kawaida, anajaribu kufikiria kama katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi tumehesabiwa bila kutoa chochote, iweje sasa unakuja kuhesabu mifugo unaanza kuweka mambo ya ada?

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishauri Serikali, kwa sababu hii imekuwa ni kero kubwa kwa wafugaji, Serikali iweze kuona ni namna gani itaendesha zoezi hili ili kila mfugaji aweze kuondokana na changamoto hiyo ya ada mbalimbali ambazo zimekuwa zikitozwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhesabu mifugo ya mwananchi na kuweka ada ni jambo ambalo limekuwa kikwazo sana kwa wananchi na Serikali inatakiwa ije na mpango mzuri ambao utawasaidia wafugaji waweze kutoa ushirikiano mzuri. Kwa sababu, kama zoezi hili litaendeshwa bure, nina imani wafugaji wote; sioni kama kuna mfugaji yeyote ambaye hatatoa ushirikiano kwenye zoezi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nasisitiza Serikali iandae utaratibu mzuri, na sidhani kama kuna mfugaji yeyote ambaye hatatoa ushirikiano kwenye zoezi hili kwa sababu, ni zoezi ambalo lina manufaa kwao kuweza kutengenezewa mazingira mazuri katika maeneo yao ya mifugo na suala zima la utoaji wa chanjo, na udhibiti wa magonjwa mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo napenda kuzungumzia, naishukuru Wizara kwa kuja na mpango mzuri wa kuzalisha nyasi kwenye mashamba makubwa kama ambavyo Mheshimiwa Waziri katusomea kwenye hotuba yake. Jambo hili ni zuri sana na litasaidia kuondokana na migogoro kati ya wakulima na wafugaji, kama endapo tutakuwa na maeneo makubwa ambayo nyasi zinazalishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kufanikisha jambo hili, ipo haja ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, na Wizara ya Kilimo, waone namna gani ambavyo watashirikiana kupitia vijana ambao wanafanya ule mradi wa Jenga Kesho Bora wa BBT, ili kuwe na coordination nzuri ambayo itasaidia Wizara, vijana hawa kupitia mafunzo wanayoyapata waweze basi kupatiwa na namna gani wanaweza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii, nami niweze kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuletea wananchi maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais, katika kipindi hiki cha Julai, 2022 hadi Machi, 2023 miradi ya kimkakati na uwekezaji amezalisha ajira 101,353, na katika ajira hizo, ajira za vijana ni 81,082. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuleta maendeleo kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi nzuri anayoifanya lakini pia na watendaji wote wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia kuhusu Kiwanda cha Vifaatiba cha Simiyu. Tarehe 11 Novemba, 2016 Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu pamoja na Mfuko wa Taifa wa Bima (NHIF), Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bohari Kuu ya Dawa (MSD), Benki ya Uwekezaji wa Maendeleo (TIB), Shirika la Utafiti wa Maendeleo ya Viwanda (TIRDO), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Dawa na TMD zilisaini randama ya makubaliano ya kuanzisha Kiwanda cha Vifaatiba zinazotokana na zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo mnafahamu, Mkoa wa Simiyu ni kinara katika uzalishaji wa zao la pamba na matarajio yetu katika mwaka huu tunategemea kuzalisha tani 300,000. Wananchi wamekuwa wakihamasika sana juu ya kuongeza uzalishaji wa zao la pamba kwa sababu waliahidiwa kuanzishwa kwa Kiwanda cha Vifaatiba. Jambo hili Wabunge wa Mkoa wa Simiyu tumekuwa tukilisemea mara kwa mara, lakini utekelezaji wake bado unasuasua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la idhini ya uanzishwaji wa kiwanda hicho uliwasilishwa kwa Wizara ya Fedha na Mipango tarehe 26 Juni, 2019, na gharama za utafiti pamoja na upembuzi yakinifu zilikuwa ni shilingi milioni 915 ambazo zilitumika katika utafiti na upembuzi yakinifu, lakini baadhi ya wataalamu walipelekwa hadi nje ya nchi kwenda kujifunza namna gani kiwanda hicho kitaanzishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, malengo ya kuanzishwa kiwanda hicho cha vifaatiba yalikuwa mawili, ambayo yamo katika andiko la mradi. Lengo la kwanza ilikuwa ni kukabiliana na soko la pamba ghafi ambazo zinaenda nje; na pili kuipunguzia Serikali mzigo wa kuagiza bidhaa zinazotokana na zao la pamba hususan upande wa Wizara ya Afya. Kama ambavyo tunafahamu, Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi sana katika uagizaji wa bidhaa hizi, ambapo ni zaidi ya shilingi bilioni 100 zimekuwa zikitumika katika uagizaji wa bidhaa hizi. Gharama ambazo zitatumika katika kuanzisha kiwanda hiki ni shilingi bilioni 75.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wazo hili, tunamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye aliubeba mradi huu kipindi akiwa Makamu wa Rais na aliubeba kama mradi ambao ni mtoto wake. Sasa tunaomba Wizara itusaidie kwa sababu mradi huu umekuwa wa muda mrefu sana na wananchi walihamasika mpaka wakatoa eneo ambalo litasaidia kuanzishwa kiwanda hiki. Mradi huu tunategemea utasaidia kutoa ajira kwa vijana, na pia utasaidia wananchi wa Mkoa wa Simiyu kuweza kuhakikisha kwamba wanaongeza thamani ya pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuongeza thamani ya pamba tutapunguza pia kuagiza vifaa ambavyo vinatokana na bidhaa zitakazotengenezwa na zao la pamba. Sasa tunamwomba Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hoja yake, aweze kutupa taarifa: Je, ni lini kiwanda hiki kitaanza rasmi? Kwa sababu wananchi wa Mkoa wa Simiyu wamekuwa wakisubiri kwa muda mrefu juu ya uanzishwaji wa kiwanda hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunamwomba Mheshimiwa Waziri, kwa sababu Mama alithamini mradi huu na ndiyo maana alikuwa kama champion kwenye huu mradi kipindi akiwa Makamu wa Rais, hivyo basi, tuna imani kubwa kwamba kama mtaufufua mradi huu naye atafurahi sana, na wananchi wote wa Mkoa wa Simiyu, wamekuwa wakiusubiri mradi huu kwa hamu kubwa sana, na pia tunatambua kwamba unaenda kutatua changamoto mbalimbali zinazotokana na zao hili la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo sina mengi ya kuzungumza, lakini nasisitiza juu ya jambo hili, juu ya uanzishwaji wa hiki kiwanda na Wabunge wenzangu wa Mkoa wa Simiyu tuna hamu kubwa sana ya kumsikiliza Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hoja yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii nami niweze kuchangia hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya. Kiupekee kabisa niipongeze Wizara ya Nishati wakiongozwa na Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa January Makamba na Naibu Waziri, Mheshimiwa Stephen Byabato na Watendaji wote wa Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Simiyu unapata umeme kutoka katika Mikoa ya jirani Mkoa wa Shinyanga, Mwanza na Mara wenye njia za umeme zenye msongo wa Kilovolt 33. Changamoto kubwa tulizonazo katika Mkoa wa Simiyu ni kiujumla njia hizi zimekuwa ni ndefu sana lakini kumekuwa na changamoto ya umeme kukatika mara kwa mara. Lakini ukiangalia Maswa Feeder ambayo ni njia ya umeme inasambaza umeme ukitoka kuanzia Kwimba, Mwanza na una-supply katika Wilaya za Bariadi tano. Sasa changamoto zikitokea katika Wilaya moja zinaathiri Wilaya zingine katika Mkoa huo. Na changamoto ya pili Mkoa huu hauna grid substation, hali hii inasababisha viwanda ambavyo vinaendeshwa katika Mkoa huu kunakuwepo na changamoto ya umeme, umeme haujitoshelezi na viwanda vingi ukiangalia tuna viwanda vikubwa saba vya pamba na vingine nane vimekufa kwa sababu ya kutokuwa na umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ya kutatua changamoto hii. Wizara ilipendekeza kuwepo na grid substation ambayo mradi ulishazinduliwa katika Kijiji cha Imalile Wilaya ya Bariadi na Mradi huu utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 75. Lakini nimeona katika bajeti fedha iliyotengwa ni Milioni 725 fedha hii ni ndogo sana na ukizingatia wananchi tayari wameshalipa fidia lakini mpaka hivi sasa bado mradi haujaanza na changamoto hii imekuwa ni ya muda mrefu sana. Tunamuomba Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hoja yake atueleze ana mpango gani na Mkoa wa Simiyu ili tuweze kupata umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine tuliyonayo katika Mkoa wa Simiyu kuna baadhi ya maeneo ya migodi ambayo hayajapelekewa umeme hadi mpakahivi sasa kwenye Wilaya ya Busega na Wilaya Bariadi. Na maeneo hayo ni kama ifuatavyo, Dutwa, Halawa, Nyawa, malamata na Bulumbaka bado yote hayajapelekewa umeme, ukizingatia migodi hii inachangia mapato ya Serikali vizuri. Kwa mfano, katika Mgodi wa Gasuma wao wanatumia zaidi ya lita 2,000 ambayo hii inaongeza gharama za uzalishaji na inasababisha wao wasiweze kuzalisha kwa kiwango cha juu. Tunaiomba Serikali iweze kupeleka umeme katika maeneo haya ili hawa wachimbaji waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye bajeti wametenga Bilioni 100 katika mradi wa kupeleka umeme katika maeneo ya wachimbaji. Nikuombe Mheshimiwa Waziri katika hiyo Bilioni 100 nasi Mkoa wa Simiyu uweze kutuona na maeneo haya ya wachimbaji yaweze kupata umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Simiyu tunavyo Vijiji 470 na Vijiji vilivyopata umeme ni Vijiji 269 na Vijiji 201 havijapata umeme. Nikuombe Mheshimiwa Waziri nimekusikia unasema utapeleka umeme kwenye Vitongoji kama huku kwenye Vijiji bado hatujaweza kufanikiwa kumaliza kupeleka umeme, nikuombe uweze kuja na mpango mzuri wa kuweza kuhakikisha kwamba Vijiji vyote vinapelekewa umeme kama tulivyoahidi katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ifikapo mwaka 2025 tutaweza kusambaza umeme katika Vijiji vyote na katika vitongoji vyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)