Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Timotheo Paul Mnzava (19 total)

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Katika Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 wananchi wa Korogwe waliahidiwa ujenzi wa barabara ya lami kutoka Korogwe - Dindira – Bumbuli.

Je, ni lini ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa barabara ya Korogwe - Dindira hadi Bumbuli inayopita kwenye maeneo yenye uzalishaji mkubwa wa mazao ya biashara na matunda imeanza kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa lengo la kujenga kwa kiwango cha lami barabara yote ya Soni – Bumbuli – Dindira - Korogwe yenye urefu wa kilomita 77 ikiwemo sehemu ya Bumbuli - Dindira - Korogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina sehemu ya Soni - Bumbuli yenye urefu wa kilomita 21.7 imekamilika mwezi Juni mwaka 2018. Hivi sasa Serikali ipo katika hatua ya ununuzi wa kumpata mtaalam mshauri wa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa sehemu iliyobaki ya Bumbuli-Dindira-Korogwe yenye urefu wa kilomita 5.3. Kiasi cha shilingi milioni 130 zimetengwa katika bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya kuanza kazi hiyo. Usanifu utakapokamilika na gharama za ujenzi kujulikana, fedha za ujenzi zitafutwa ili ujenzi wa kiwango cha lami uanze kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Wananchi wa Tarafa ya Mombo wamekuwa na hitaji la kuwa na skimu kubwa ya umwagiliaji katika Bonde la Mto Mkomazi na mara kadhaa viongozi wa Serikali wamekuwa wakitoa ahadi ya kukamilisha jambo hilo.

Je, ni lini Serikali itatekeleza mradi wa umwagiliaji katika Bonde la Mto Mkomazi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Mnzava Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijiji kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka 1980 Serikali kupitia na washirika wa maendeleo, yaani Wakala wa Ushirikiano wa Kitaalam wa kimataifa wa Serikali ya Ujerumani (Germany) Agency for Technical Cooperation Limited) ulifanya upembuzi yakinifukwa ajili ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Mkomazi katika tarafa ya Mombo, Halmashauri ya Korogwe. Hata hivyo taarifa ya upembuzi yakinifu na usanifu zilibaini kuwa ujenzi wa bwawa hilo ungesababisha kuongezeka kwa maji katika Ziwa Manga na kupelekea kuzama kwa Kijiji cha Manga Mikocheni pamoja na mashamba ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto hiyo katika mwaka 2014/2015 wataalam wa Ofisi ya Kanda ya Umwagiliaji ya Kilimanjaro walifanya mapitio ya upembuzi yakinifu upya na usanifu wa kina uliofanywa katika eneo hilo kwa lengo la kuepusha uwezekano wa kufurika kwa Ziwa Manga, kuzama kwa Kijiji ca Manga Mikocheni na mashamba ya wakulima kutokana na ujenzi wa bwawa hilo. Mapitio hayo yalibaini uwezekano wa ujenzi wa bwawa na mradi wa umwagiiaji katika eneo hilo bila kuathiri wakazi wa eneo hilo. Mapitio ya usanifu huo yalibaini kuwa ujenzi wa bwawa pekee utagharimu shilingi bilioni 1,543,736,877.

Mheshimiwa Spika, Serikali iko katika mchakato wa kufanya ukaguzi na tathmini ya kina ya miradi yote ya umwagiliaji nchini ili kufanya uhakiki wa eneo la umwagiliaji kwa lengo la kubaini ubora wa miradi, thamani ya fedha, gharama za miradi na mahitaji halisi ya sasa ya kuboresha, kuendeleza na kuongeza miradi mipya ya umwagiliaji. Aidha, baada ya tathmini hiyo Serikali itaendelea kutafuta fedha ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha mabwawa na skimu za umwagiliaji nchini ikiwemo mradi wa umwagiliaji katika Bonde la Mkomazi zinaendelezwa na kuwanufaisha wananchi wa Mombo na taifa kwa ujumla.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Katika Jimbo la Korogwe Vijijini bado vijiji vingi havina umeme.

Je, ni lini usambazaji wa umeme kupitia REA utakamilika katika vijiji vya Jimbo la Korogwe Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kutekeleza mradi wa kupeleka umeme katika vijiji vyote nchini hadi ifikapo mwezi Juni, 2021. Katika Jimbo la Korogwe Vijijini jumla ya vijiji 71 vitaunganishiwa umeme. Aidha, vijiji 14 vya Hamashauri ya Wilaya ya Korogwe Vijijini vinatarajiwa kupatiwa umeme kupitia Mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea kutekelezwa. Hadi kufikia mwezi Juni, 2019 Mkandarasi Kampuni ya DERM Electrics ameshawasha umeme katika vijiji vinne vya Nkalekwa, Magila, Kwasunga na Welei pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali zaidi ya 112.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa mkandarsi anaendelea na kazi ya kusimika nguzo, kuvuta nyaya na kufunga transifoma katika vijiji kumi vitakavyopatiwa umeme kupitia mradiwa REA lll mzunguko wa kwanza. Kazi za mradi katika Jimbo la Korogwe Vijijini zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 9.45, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 48 na ufungaji wa transfoma 18 za kVA 50 na 100, pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali 825 na gharama za mradi ni shilingi bilioni moja na milioni 600.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyosalia 57 vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili, unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Barabara ya Msambiazi - Lutindi – Kwabuluu ni muhimu kwa uchumi na maisha ya watu wa Korogwe hususan Kata za Tarafa ya Bungu, lakini barabara hii ni mbovu na korofi sana.

(a) Je, ni lini Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami?

(b) Je, ni lini barabara hii itapandishwa kuwa ya mkoa hasa ikizingatiwa kuwa inakwenda kuunganisha Bumbuli na Lushoto?
WAZIRI WA NCHI, OFISI WA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, barabara ya Msambiazi – Lutindi – Kwabuluu ni barabara ya Mkusanyo (Collector road) yenye urefu wa kilometa 17.5. Kuanzia Mwaka wa Fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali imeifanyia matengenezo kwa gharama ya shilingi milioni 43. Katika Mwaka wa fedha 2020/2021 Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) Wilaya ya Korogwe umeomba kutengewa shilingi milioni 50 kwa ajili ya matengenezo ya barabara hii. TARURA Wilaya ya Korogwe inaendelea kufanya upembuzi wa kina wa mtandao wa barabara zake utakaobaini vipaumbele vya ujenzi wa mtandao wa barabara Wilayani Korogwe kwa viwango vya lami, changarawe na vumbi.

(b) Mheshimiwa Spika, kabla ya kuanzishwa kwa TARURA, barabara hii iliombewa kuingizwa kwenye orodha ya barabara zinazohudumiwa na TANROADS kupitia Baraza la Madiwani ambapo baada ya kuanzishwa kwa TARURA imepewa jukumu la kuendelea kuihudumia barabara hiyo. Aidha, Serikali imeshatoa maelekezo kwa Makatibu Tawala wa Mikoa yote nchini kuhusu utaratibu wa Bodi za Barabara za Mikoa, Wabunge au Kikundi cha watu kutuma maombi ya kupandishwa hadhi barabara. Utaratibu huu umetolewa na Kamati ya Kitaifa ya Kupanga Barabara katika Hadhi Stahiki (National Roads Classification Committee- NRCC).
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya muda mrefu ya Mhe. Rais ya ujenzi wa Bwawa la umwagiliaji kwenye Bonde la Mto Mkomazi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali Mheshimiwa Timetheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Skimu ya Umwagiliaji ya Mkomazi ipo katika Kijiji cha Manga Mikocheni, Kata ya Mkomazi, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe. Skimu hiyo ina jumla ya hekta 5,000 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji ambapo kati ya hizo, hekta 200 zimeendelezwa kwa kujengewa miundombinu ambazo zilifadhiliwa kutokana na fedha za ndani za halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Kilimo kupitia Ofisi ya Tume ya Umwagiliaji ilifanya mapitio ya upembuzi yakinifu ya awali na kubaini hitaji la Sh.3,379,000,000 ili kuendeleza bonde hilo. Kati ya fedha hizo Sh.4,041,000,000 ni kwa ajili ya ujenzi wa bwawa na Sh.2,337,999,000 ni za ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji. Ujenzi wa Skimu ya Mkomazi pamoja na bwawa lake upo katika Mpango wa Umwagiliaji wa mwaka 2018 (National Irrigation Master Plan). Mkakati mpana wa Serikali ni kuendeleza miundombinu ya umwagiliaji ili ifikapo mwaka 2025 tuwe na uwezo wa kumwagilia hekta milioni 1.2 ambapo Skimu ya Mkomazi ni mojawapo ya skimu zitakazotekelezwa katika mkakati huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Wizara imeanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Umwagiliaji wenye lengo kufanya matengenezo ya miundombinu na kujenga miradi mpya. Pia Wizara imeelekeza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kuanzia sasa kujenga miradi kwa kutumia wataalam wa ndani kwa utaratibu wa force account kwa Mfumo wa Usanifu na Ujenzi (Design and Build).
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya upungufu wa watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe hasa kwenye Idara za Afya, Elimu na Kilimo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Tawala za Miko ana Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ikama ya mwaka 2020/2021, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe inapaswa kuwa na watumishi 2,630. Hadi Machi 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe ilikuwa na watumishi 2,294 hivyo ina upungufu wa watumishi 336 sawa na asilimia 12.8.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ikama Idara ya Afya katika Halmashauri ya Wlaya ya Korogwe inapaswa kuwa na watumishi 392, na hadi Machi 2021 Idara ya Afya ilikuwa na watumishi 263 hivyo ina upungufu wa watumishi 129 sawa na asilimia 32.9. Idara za Elimu msingi na sekondari zinapaswa kuwa na watumishi 1891 lakini zina watumishi 1604 hivyo zina upungufu wa watumishi 287 sawa na asilimia 15.2. Idara ya Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika inapaswa kuwa na watumishi 55 na ina watumishi 45 hivyo ina upungufu wa watumishi 10 sawa na asilimia 18.2.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeendelea kuajiri na kuwapnaga watumishi wa kada mbalimbali katika halmashauri nchini ambapo katika mwaka wa fedha 2020/21 watumishi 81 wapya waliajiriwa na kupangwa katika Halamshauri ya Wilaya ya Korogwe. Kati ya hao, watumishi 22 ni walimu wa sekondari, 35 shule za msingi, 6 watumishi wa kada za afya na Afisa Ugani 1 pamoja na 17 wa kada mbalimbali. Pamoja na jitihada hizo, katika Ikama ya mwaka 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya imetenga nafasi za ajira mpya 150 ambao watapangwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha kazi ya kupeleka umeme vijiji 49 vya Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe ambavyo bado haijapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 49 vilivyobaki katika Wilaya ya Korogwe ilianza mwezi Mei, 2021 na kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika ifikapo mwezi Septemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya utekelezaji wa mradi huu inahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 urefu wa kilometa 289.4, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 urefu kilometa 45, ufungaji wa transfoma 50 zenye uwezo wa KVA 50 pamoja na kuunganisha huduma ya umeme wateja wa awali 990. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 12.85.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italifuta shamba la Mwakinyumbi Estate lililotelekezwa kwa muda mrefu na kuwapa wananchi wa Hale na maeneo jirani ili waweze kufanya shughuli za kiuchumi?
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Shamba la Mwakinyumbi Estate lilimilikishwa kwa barua ya toleo yenye Kumb Na. TRKF/76/ 65/AOM kwa muda wa miaka 99 toka tarehe 1 Aprili, 1989 kwa matumizi ya kilimo. Mmiliki alipewa masharti ya umiliki kwa mujibu wa Sheria za Ardhi. Miongoni mwa masharti hayo ni uendelezaji wa shamba na ulipaji wa kodi ya pango la ardhi kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, ukaguzi uliofanyika wa ndani umebaini kuwa shamba hilo limetelekezwa na hakuna uendelezaji wowote uliofanyika na kwa sasa shamba hilo linadaiwa kiasi cha shilingi milioni 174.73 ikiwa ni kodi pamoja na malimbikizo kwa muda wa miaka 17 kuanzia mwaka 2005 hadi mwaka huu 2021. Kutokana na hali hiyo, Serikali ilianza kuchukua hatua za kisheria za kubatilisha miliki ya shamba husika kwa kutuma ilani ya kusudio la ubatilisho wa milki kwa siku tisini (90). Mmiliki hakuwasilisha utetezi wowote juu ya ilani ya ubatilisho aliyotumiwa kufuatia uvunjaji wa masharti kama ilivyoainishwa katika barua yake ya toleo. Hivyo, Serikali kwa sasa inaendelea na hatua za ubatilisho hatua zilizobaki mimi naandika barua kwa Mheshimiwa Rais kumshauri shamba hilo afute.

Mheshimiwa Spika, naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, ufutaji wa mashamba yaliyotelekezwa nchini ni zoezi endelevu kwa mujibu wa sheria ikiwa na lengo la kulinda maslahi mapana ya Taifa, wananchi na wawekezaji. Hatua hii inapunguza migogoro ya matumizi ya ardhi ambayo imekuwa ikijitokeza katika maeneo mbalimbali nchini.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua Kiwanda cha Tembo Chipboard kilichopo Kata ya Mkumbara Wilayani Korogwe?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Tembo Chipboards Limited ni kiwanda kilichokuwa kikimilikiwa kwa ubia kati ya Serikali ikiwa na hisa asilimia 80 na Kampuni ya Grewalls Saw Mills asilimia 20. Mnamo tarehe 13 Aprili, 2004 Serikali ilibinafsisha kiwanda hicho kwa kuuza hisa zake zote asilimia 80 kwa mwekezaji wa kampuni ya MELJON Bf ya Uholanzi na baadaye tarehe 13 Machi 2015 Kampuni ya Grewalls Saw Mills ilisaini makubaliano na MELJON Bf kwa kuuza hisa zake asilimia 20. Hivyo kampuni ya MELJON Bf iliendelea kuwa mmiliki wa kiwanda kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, kufuatia zoezi la ubinafsishaji wa viwanda, mwekezaji MELJON Bf alitakiwa kuwekeza kulingana na mkataba. Kutokana na uwekezaji huo kutofanyika, tarehe 16 Oktoba, 2018 Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina ilifanya maamuzi ya kukirejesha kiwanda na mwekezaji alipewa barua ya kuvunja mkataba.

Mheshimiwa Spika, Msajili wa Hazina anamalizia taratibu za kukirejesha kisheria kiwanda hiki Serikalini. Urejeshaji huu ukikamilika ndipo uwekezaji mpya utafanyika ili kuwezesha kukifufua kiwanda hicho. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakarabati Kituo cha Afya Bungu Wilayani Korogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Bungu ni kikongwe, chakavu na kipo kwenye eneo finyu. Serikali imefanya tathmini na kuweka mpango wa kujenga kwa awamu Kituo cha Afya kipya kwa gharama ya shilingi milioni 400.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe katika mwaka wa fedha 2023/2024 itatenga kutoka mapato ya ndani shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Bungu. Aidha, Halmashauri itaendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo hicho. Ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO K.n.y. MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia upatikanaji wa chakula cha bei nafuu kwa wananchi walioathirika na ukame nchini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) imeendelea kutoa chakula na kukiuza chini ya bei ya soko. Hadi kufikia tarehe 31 Januari, 2023, kiasi cha mahindi tani 24,975 zimepelekwa na kuuzwa katika Halmashauri 60 nchini katika vituo vya mauzo 116. Katika Halmashauri ya Korogwe, kituo cha mauzo kimefunguliwa eneo la Masewa tarehe 27 Januari, 2023. Jumla ya tani 32 zimepelekwa na tani 10 zimeshanunuliwa.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya Korogwe – Dindira – Bumbuli hadi Soni ambayo ilitengewa fedha kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi katika mwaka wa fedha 2020/2021?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu na Usanifu wa Kina kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami Barabara ya Korogwe – Dindira – Bumbuli – Soni (km 77) unafanyika kwa awamu. Sehemu ya kutoka Soni hadi Bumbuli (km 21.7) upembuzi yakinifu na usanifu wa Kina umekamilika. Kwa Sehemu iliyobaki ya kutoka Bumbuli hadi Korogwe (km 55.3), kazi ya Upembuzi Yakinifu na Usanifu wa Kina inaendelea na imefikia asilimia 81.

Mheshimiwa Spika, baada ya Kazi ya Upembuzi Upembuzi yakinifu na Usanifu wa Kina kukamilika na gharama za ujenzi kujulikana, Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kusaidia kuongezeka kwa bei ya zao la chai kwa wakulima nchini?
WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bei ya zao la chai hutegemea mwenendo wa Soko la Dunia, soko la ndani na ubora wa chai sokoni. Serikali inatekeleza mikakati mbalimbali kuhakikisha uwepo wa mazingira bora yanayoleta ushindani ili kuchochea bei ya chai. Katika hatua ya awali, kwa mwaka 2023 bei ya chai imeongezeka kutoka shilingi 312 hadi shilingi 366 kwa kilo. Aidha, mikakati mingine ya kupandisha bei ni kuongeza uzalishaji wa miche bora ya chai, kuendelea kuhamasisha matumizi ya chai nchini, kuanzisha mnada wa chai, kutoa ruzuku ya mbolea na miche bora ya chai ili kuongeza tija na uzalishaji na kuandaa mwongozo wa ubora wa majani mabichi ya chai na kuanzisha kiwanda cha kusindika chai maalumu.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Kata za Mkalamo, Magamba Kwalukonge na Mkomazi Wilayani Korogwe?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua adha ya maji inayowakabili wananchi wa Kata za Mkalamo, Magamba, Kwalukonge na Mkomazi Wilayani Korogwe. Hatua mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa kukabiliana na hali hiyo na katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imechimba visima viwili virefu, kufunga pampu na kujenga tenki la lita 75,000 ambapo wananchi wa vijiji vya Magamba, Kwalukonge, Changalikwa na Makole Kata ya Magamba Kwalukonge wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa Kata zilizobaki, Serikali itajenga miradi ya maji kupitia chanzo cha Mto Pangani, Mtaalam ameajiriwa na anaanza kazi mwezi Mei, 2023 na utekelezaji wa miradi utafanyika katika mwaka wa fedha 2023/2024.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, lini barabara ya Mombo Mzeri itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Mombo - Mzeri ina urefu wa jumla ya kilometa 30 inayounganisha barabara kuu ya Segera – Same na Makao Makuu ya Kata ya Magambakwalukonge, Mkalamo na Wilaya ya Handeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaanza kufanya Upembuzi yakinifu na Usanifu wa kina katika barabara hii na kazi hii inatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 ili kupata gharama halisi za ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA imeendelea kuimarisha barabara hii kwa kiwango cha changarawe pamoja na kujenga vivuko na makalavati ili kuhakikisha inapitika majira yote ya mwaka.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha bei ya Zao la Mkonge haitetereki?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA K.n.y WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha bei ya zao la mkonge haitetereki, Wizara ya Kilimo kupitia Bodi ya Mkonge imechukua hatua mbalimbali ikiwemo kuimarisha soko la ndani kwa kuongeza matumizi ya ndani katika kutengeneza bidhaa zilizoongezwa thamani kama vile kamba, mazulia, magunia, mapambo na bidhaa za ufumaji na kupunguza matumizi ya bidhaa kutoka nje kama uagizaji wa kamba za plastiki, mazulia na vifungashio.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea kutenga bajeti kila mwaka kuanzia mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya kununua mashine mpya za kuchakata (makorona) ili kuhakikisha kuwa, ubora wa mkonge unaochakatwa unakidhi matakwa na viwango vya soko la ndani na soko la kimataifa na hivyo kuimarisha bei ya zao hilo, nakushukuru sana.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Je, lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga barabara za lami katika Mji wa Mombo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022, TARURA ilitenga jumla ya kiasi cha shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuchonga na kuweka changarawe urefu wa kilometa 2.7, kujenga makalavati tisa, kujenga mifereji yenye urefu wa kilometa 1.9. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga jumla ya Shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuchonga kilometa 2.84 kwa kuweka changarawe, ujenzi wa makalavati 23 na ujenzi wa mifereji urefu wa kilometa 2.46. Utekelezaji wa kazi hizi unaendelea na umefikia asilimia 56. Kwa mwaka wa fedha 2023/2024 jumla ya shilingi milioni 200 zimetengwa kwa ajili ya barabara hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za Mombo Mjini zitaanza kujengwa kwa kiwango cha lami mara baada ya kuziimarisha kwa kiwango cha changarawe na ujenzi wa mifereji kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, lini Serikali itavigawa Vijiji vya Makangara, Mkomazi, Mkalamo, Mwenga, Kwemasimba, Mkwajuni, Sekioga na Bungu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uanzishaji wa maeneo ya utawala hutekelezwa kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa Sura Na. 287 na Na. 288 pamoja na mwongozo wa uanzishaji wa maeneo ya utawala wa mwaka 2014 ambao umeanisha utaratibu na vigezo vinavyopaswa kufuatwa. Miongoni mwa vigezo hivyo ni uwezo wa Halmashauri kujitegemea katika bajeti ya uendeshaji kutokana na mapato ya ndani, uwezo wa kutoa huduma za kijamii na kiutawala, upatikanaji wa huduma za mawasiliano ya simu na uwepo wa huduma ya umeme.

Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa kipaumbele kuboresha na kukamilisha miundombinu msingi kwenye maeneo yaliyoanzishwa ili yaweze kutoa huduma kwa jamii na baadae kuendelea na maeneo mengine kwa kufuata taratibu na vigezo vilivyoainishwa.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kuboresha na kupanua Vituo vya Afya vya Bungu, Magama na Mombo ambavyo vinahudumia wananchi wengi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza ujenzi wa vituo vya afya kote nchini ikiwemo katika Jimbo la Korogwe Vijijini. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imepeleka shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya Mnyuzi na Kerenge katika Jimbo la Korogwe Vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Vituo vya Afya vya Mombo, Bungu na Magoma Serikali inafanya tathmini ya vigezo stahiki kwa ajili ya kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji.