Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kiza Hussein Mayeye (13 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii . Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uzima, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kukurudisha salama na afya yako inaendelea kuimarika, hakika neno la Bwana lihimidiwe siku zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nichangie katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwasilisha hotuba yake vizuri kwa sababu inaeleweka. Nimeisoma na nimeielewa vizuri. Sasa naomba nianze kuchangia katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada zote ambazo zinafanywa na Serikali yetu, lakini bado katika suala zima la afya, changamoto ni kubwa, wauguzi wamekuwa ni changamoto kubwa. Katika maeneo ambayo natokea, Mkoa wa Kigoma hospitali nyingi hazina wauguzi. Hata hivyo, pamoja na kwamba hazina wauguzi hata miundombinu ya hospitali hizo bado ni changamoto. Waganga wanaishi katika mazingira magumu, nyumba za Waganga hakuna. Niiombe sana Serikali ijitahidi kuzingatia hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndani ya Mkoa wangu wa Kigoma tuna Hospitali ya Mkoa ambayo inaitwa Maweni. Hii ni hospitali kubwa ambayo inahudumia wananchi wengi na ukizingatia Kigoma tuko mpakani ambako tunapokea wakimbizi kutoka Burundi na Congo bado wanakwenda wanatibiwa mahali pale. Niiombe sana Serikali ituletee ma- specialist ndani ya Mkoa wetu wa Kigoma katika hospitali hii ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa uchunguzi ambao nimeufanya, mpaka sasa tuna-specialists watatu. Specialist wa akinamama, wa upasuaji na watoto. Niiombe sana Serikali mtuongezee ma-specialist katika hospitali yetu ya mkoa. Kwa sababu leo unapoweka specialist mmoja katika upasuaji naye ni mwanadamu ana dharura, kesho asipokuwepo kazini maana yake unawaambia watu wa Kigoma hamtakiwi kufanyiwa upasuaji. Niiombe sana Serikali ituletee wauguzi, ituletee waganga katika hospitali zetu.

Mheshimiwa Spika, nimetembelea katika vijiji mbalimbali ndani ya Wilaya yangu ya Kigoma Vijijini. Nimekwenda Vijiji vya Kiziba, Mwamgongo na Bugamba, kuna changamoto kubwa. Usafiri wanaoutumia ni kupita na boti ndani ya maji. Tuangalie katika maisha ya kawaida mama huyu mjamzito anahitaji operation ya haraka, lakini hakuna boti ya haraka ya kuweza kumtoa Bugamba au Mwamgongo kumpekea hospitali ya Maweni. Niiombe sana Serikali iwaangalie watu wa pale angalau tupate boti ambayo litawasaidia wananchi wa maeneo haya kuwasafirisha kwenda katika hospitali ya mkoa.

Mheshimiwa Spika, niiombe tena Serikali; natokea katika Wilaya ya Kigoma Vijijini, lakini mpaka sasa hatuna hospitali ya Rufaa; tuna vituo viwili vya afya ambavyo ni; Bitale, Nyamasovu ambacho ni cha mission na kingine kinajengwa Mwamgongo ambacho Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya amekifungua mwezi uliokwisha. Niombe sana Serikali mtuangalie Wilaya ya Kigoma Vijijini tuweze kupata hospitali hii ya wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala zima la vifaa. Hospitali ya Mkoa wa Kigoma na maeneo mengine yote ya Tanzania, hospitali hizi zinakabiliwa na kukosa vifaa. Leo unapokwenda katika hospitali ya Mkoa wa Kigoma hakuna CT-Scan machine inalazimu mtu apewe rufaa kutoka Kigoma kwenda Bugando, kutoka Kigoma kwenda Muhimbili; hali hii inasababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi. Niiombe Serikali tupate vifaa hivyo katika hospitali zetu na tuweze kuwasaidia wananchi wetu wapate huduma ndani ya mikoa yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala zima la barabara. Maeneo mengi ndani ya nchi yetu barabara bado ni changamoto kubwa. Nirudi kule kule katika Mkoa wangu wa Kigoma tuna barabara ambayo inatoka Mwandiga – Bubango – Chankele inakwenda Kagunga ambayo tunasema ni Kagunga Road.

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali itusaidie barabara hii iingie katika Mpango, iwekwe kiwango cha lami iweze kuwasaidia wananchi hawa ambao maisha ya yamekuwa ni kupita katika maji, wanahatarisha maisha yao na wao waweze kutumia usafiri wa barabara. Kwa hiyo niiombe sana Serikali, barabara hii muweze kuisaidia tuipate. Itatusaidia sana na wananchi hawa na wataweza kutoka sehemu moja na kwenda sehemu nyingine pasipokuwa na wasiwasi wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la TARURA. Wananchi wengi hawana uelewa kuhusu TARURA. Natokea katika Kijiji cha Mwandiga, wengi hawaelewi TARURA wanafanya kazi gani na hata mimi nilikuwa nashangaa, kwa nini barabara hizi za mitaa hazifanyiwi kazi, nikajua ni TANROADS lakini nikaambiwa sasa zimekwenda kwa TARURA. Niiombe sana Serikali iwasaidie TARURA bajeti ipatikane, barabara hizi zitengenezwe.

Mheshimiwa Spika, vile vile nishauri TARURA washirikiane na watu kama Waheshimiwa Madiwani ili waweze kuwapa vipaumbele wajue ni barabara gani wanatakiwa wazianze, ni barabara gani za vipaumbele wazifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana Serikali ifanyie kazi hilo. Pia niongelee barabara ya kutoka Kidahu – Nyakanazi. Hii barabara ni potential, ni barabara muhimu sana. Kwa taarifa nilizonazo mkandarasi yuko pale lakini barabara hii inasuasua. Nimeipita nilikuwa nikitembea katika Vijiji vya Pamila, nimepita barabara ile, unakuta hapa pamechimbwa, hapa pamechimbwa, inaonekana mkandarasi yuko slow. Niiombe sana Serikali itusaidie barabara ile imalizike kwa wakati na kazi ziendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee tena katika uwezeshaji wa wananchi kiuchumi. Katika ukurasa wa 14 wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu anasema kwamba kuna pesa ambazo zimetengwa katika SACCOS lakini pia katika vikundi vya akina mama zaidi ya bilioni 3.4 katika Halmashauri 53. Ningeomba ufafanuzi; hizi halmashauri ambazo hizi pesa zimekwenda ni zipi? Kwa sababu leo katika Halmashauri yangu ya Kigoma Vijijini kuna vikundi vya akinamama, kuna vikundi vya walemavu, kuna vikundi vya vijana lakini bado hawajapatiwa pesa hizo. Niombe kufahamu, halmashauri hii haijapata na kama pesa zimefika zimetumikaje au wanapewa akinamama wa mjini tu na sio akinamama vijijini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niiombe sana Serikali iwaangalie akinamama, vijana na walemavu, kwa sababu naamini ukimwezesha mama umeikomboa jamii; na vijana wa Kitanzania wanataka ajira, ajira imekuwa ni changamoto. Tuwawezeshe mitaji waweze kufanya kazi ili wasikae vijiweni ambako matokeo yake ni kuvuta bangi na kuingia katika biashara ya kujiuza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine niongelee suala zima la reli. Nimefurahishwa sana na Serikali kwamba, inakwenda kuanzisha huu mradi wa standard gauge. Ni mradi mzuri, tuuunge mkono, lakini ningeomba sana usiishie katika Mkoa wa Tabora, ufike mpaka Kigoma, tunahitaji standard gauge ndani ya Kigoma. Kwa sababu, naamini kabisa ikifika Kigoma tutakuza uchumi wa nchi, tutakuza uchumi wa Kigoma. Leo Kigoma tayari tumepata bandari kavu ya Katosho, naamini kama standard gauge itafika Kigoma, Wakongo, Warundi, magari ambayo watayaleta katika bandari ile ya Kigoma watatumia reli hii ya standard gauge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba, Kigoma na sisi tupate hii standard gauge ningeomba sana hii metre gauge, reli hii ya kati, Serikali iboreshe miundombinu. Changamoto ni kubwa, asilimia 90 ya wananchi wa Kigoma tunategemea usafiri wa reli ya kati. Wengi hawana uwezo wa kupanda ndege, wengi hawana uwezo wa kupanda mabasi haya kwa Sh.60,000/= wanakimbilia huku kwenye treni ya Sh.18,000/= lakini miundombinu ni mibovu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Kigoma unaambiwa terni itaondoka saa 2.00 asubuhi, lakini unakuja kuondoka saa
8.00 usiku. Wale walioko pale abiria ni akinamama, watoto, kuna wagonjwa, kuna wajawazito. Wengine wametoka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema. Vilevile nipende kukupongeza Mheshimiwa Waziri wa Elimu, mama yangu, Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako, kwa jitihada na kazi unayoifanya katika kuhakikisha elimu yetu inapiga hatua mbele. Lakini pamoja na jitihada za Serikali, bado sekta ya elimu ina changamoto kubwa sana, hivyo kwa bajeti ambayo imetengwa hamtaweza kumaliza changamoto zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mishahara ya walimu; walimu ni watu muhimu sana katika maisha yetu kwani wote tumefika hapa tulipo kutokana na walimu, lakini leo hii mwalimu anaonekana kama hana thamani na ni kazi ya waliofeli kuwa waimu wa shule za msingi kwani mishahara wanayopata ni midogo sana kiasi kwamba walimu wanaishi kwa shida na pesa wanayopata ni ndogo sana. Niiombe sana Serikali, mwalimu apewe kipaumbele, aongezewe mshahara ili naye afurahie kazi yake. Walimu wengi hawafurahii kazi ya ualimu, wanafanya kwa shida tu kutokana na wanachokipata kuwa kidogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa miundombinu ya shule zetu; shule nyingi hazina miundombinu mizuri vijijini na hata mijini, madarasa mengi hayapo katika mazingira mazuri, wanafunzi wanateseka sana kwani hata vyoo vya shule zetu nyingi bado ni changamoto kubwa. Sasa tujiulize hawa watoto wanasomaje bila kuwa na vyoo? Kwa hali hii lazima watoto hawa wataendelea kupata magonjwa kama kipindupindu. Lakini hata vyoo ambavyo vipo ni vichafu sana, hakuna hata maji, niiombe sana Serikali iweke maji katika shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule zetu nyingi hakuna madarasa ya kutosha, watoto wanasoma chini ya miti, jua na mvua, vyote vyao. Ninaiomba sana Serikali ijenge madarasa ya kutosha. Kwa mfano katika Wilaya ya Kigoma Vijijini, shule nyingi hazina madarasa ya kutosha, kama vile shule za Nkema, Mwandiga, Nyamhoza, Kizenga, Bugamba, Kiziba na Nyamigura madarasa ni machache sana, lakini vyoo hakuna, madawati hakuna. Niiombe sana Serikali iweke miundombinu ya shule zetu kuanzia katika madarasa, madawati, vyoo na vifaa vya kufundishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu watoto wenye mahitaji maalum; watoto hawa katika suala la elimu bado wamesahaulika sana, kwani bado shuleni hawapo wengi lakini pia miundombinu ya shule zetu bado inambagua mtoto mlemavu. Watoto hawa hawana vifaa vyao maalum na vilevile walimu wa watoto hawa bado ni wa kutafuta, vyoo vilivyopo watoto hawa wanapata shida sana kutumia kutokana na jinsi vilivyojengwa, havimpi support mlemavu huyu ili aweze kuvitumia. Wapo watoto hawawezi kutembea kabisa, wanatambaa na vyoo ni vichafu sana, hakuna maji, tunamuweka mtoto huyu katika hali gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Mwandiga, Kigoma Vijijini kuna shule ya Nkema, ina watoto walemavu lakini shule hii haina madarasa, vyoo, watoto hawa wanapata shida kubwa, walimu wa watoto hawa hakuna. Niombe sana Serikali iwajali watoto hawa kuanzia katika vifaa, walimu, miundombinu ya ujenzi, madarasa na vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu chombo cha kusimamia elimu; kama kweli tunataka kupandisha hadhi elimu yetu, ni muhimu Serikali iunde chombo kimoja ambacho kitakuwa na kazi ya kusimamia elimu yetu. Chombo hiki kiwe maalum kwa kuangalia elimu yetu, kiweke mikakati ya kuhakikisha elimu yetu inapiga hatua; chombo hiki kisimamie kuanzia ngazi ya shule za msingi mpaka vyuo vikuu, hii itatusaidia sana kuboresha elimu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upandishaji madaraja kwa walimu; hii imekuwa changamoto kubwa sana kwa walimu. Serikali imekuwa ikipandisha walimu madaraja kutoka daraja moja A kwenda B, lakini mwalimu huyu anaishia kupata barua tu, stahiki zake kama ongezeko la mshahara hapati kwa wakati na wapo ambao wamestaafu lakini mafao yake amepigiwa hesabu kwa daraja A wakati alipanda daraja miaka 16 iliyopita; hii siyo haki kabisa. Kiukweli walimu wanateseka sana na jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali mtu apewe stahiki yake mara tu aapopanda daraja, kama ametokea daraja A mwezi Mei, basi mwezi huo huo apokee mshahara wake wa daraja jipya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu michezo ya UMITASHUMTA, michezo ni uhai kwani hujenga afya na vilevile hutengeneza mahusiano mazuri ya ujirani mwema. Lakini sasa hivi michezo hii haina nguvu, imesahaulika sana. Niombe sana Serikali irudishe michezo shuleni, inasaidia sana wanafunzi kiafya, kimwili na kiakili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu walimu wa sayansi, hili limekuwa tatizo sugu, shule zetu hazina walimu wa sayansi, hii inafanya wanafunzi kuchukia masomo ya sayansi, sasa kama tunataka kuwa nchi ya viwanda ni lazima tuweke walimu wengi wa sayansi ili tupate wataalam wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, muumba wa mbingu na ardhi kwa kunipa uzima na afya tele na kunifikisha mahali hapa siku hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nikishukuru chama change, Chama cha Wananchi (CUF) chini ya Mwenyekiti mahiri Profesa Ibrahim Lipumba pamoja na Naibu Katibu Mkuu Mheshimiwa Magdalena Sakaya kwa kusimamia vizuri Katiba ya Chama cha Wananchi (CUF). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe shukrani zangu za dhati kwa Wabunge wote wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano, kutupokea vizuri, kuwa pamoja na sisi, kutuelekeza na kutufundisha mambo mbalimbali toka tulivyoingia Bungeni mpaka siku hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri Dkt. Phillip Mpango kwa Mpango huu wa Maendeleo, Mpango huu ni mzuri lakini haimaanishi kila kitu kizuri hakina kasoro. Kwa hiyo, mimi nimpongeze lakini pia naomba nichangie kama ifuatavyo katika Mpango huu wa Maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa kwanza nataka nianzie katika suala zima la hawa wawekezaji. Serikali yetu inasisitiza na inasema kwamba tunahitaji wawekezaji. Kwa hiyo, ningeomba Serikali yetu iwape wawekezaji uwezo wa kuja kuwekeza katika maeneo mbalimbali katika nchi yetu ya Tanzania. Kuna maeneo ambayo kwa mfano ninakotoka Mkoa wa Kigoma, huu ni mkoa ambao uko katika plan hii ya Regional Economic Zone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kigoma mpaka sasa kuna zaidi ya heka 690 katika eneo la Kisezi ambalo limetengwa kwa shughuli hizi za uchumi. Ningemuomba Mheshimiwa Waziri, mhakikishe kwamba mnavutia wawekezaji katika eneo hili kwa sababu eneo hili ni potential, ni eneo ambalo tukilitumia vizuri kwa uchumi tutainua Pato la Taifa na hata mkoa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimwambie Mheshimiwa Waziri katika eneo hili la Kisezi tayari kuna mwekezaji ambaye anatengeneza umeme wa jua na mpaka sasa ameshatengeneza megawati tano, lakini kuna ukwamishaji. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, kama Serikali yetu inasema kwamba inatoa kipaumbele katika sekta binafsi ihakikishe umeme huu wa jua ambao mwekezaji huyu ameuweka katika eneo lile uweze kuunganishwa na TANESCO Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme huu TANESCO wanakataa kuunganisha, lakini mpaka leo Kigoma hatujaingia katika Gridi ya Taifa. Ningeomba tuingie katika mpango wa Gridi ya Taifa na sio Kigoma tu bali ni Mikoa yote ya Magharibi ikiwepo Sumbawanga, Katavi na Kigoma. Kwa hiyo, naomba katika Mpango huu mhakikishe kwamba mikoa hii tunaingia katika Gridi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia TANESCO Kigoma wanasema kwamba hawawezi kuunganisha umeme huu lakini katika akili ya kawaida unajiuliza ni kwa nini hawataki? Kwa sababu kama mwekezaji huyu anatumia shilingi 490 kwa unit moja TANESCO Kigoma inatumia shilingi 700 ka unit moja kwa akili ya kawaida unaona kabisa kwamba mwekezaji huyu umeme wake uko chini. Ni kwa nini Serikali haitaki mwekezaji huyu umeme wake uunganishwe TANESCO Mkoa wa Kigoma? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika maeneo yale ambayo Serikali imeyatenga kama maeneo ya maendeleo, nirudi Kigoma. Kigoma mpaka dakika hii bandari kavu imeanzishwa, hii Central Corridor, Umoja wa Nchi za Maziwa haya Makuu wamefikia uamuzi kwamba Kigoma iwe ni bandari ya mwisho kwa mantiki kwamba watu kutoka Burundi, Kongo badala ya kufuata mizigo Dar es Salaam wataweza kuifuata Kigoma na tayari eneo limetengwa la Katosho – Kahagwa, tunatengeneza kitu tunasema CIF Kigoma. Kwa hiyo, tutakuwa na bandari kavu pale na tayari watu wamepisha ujenzi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri katika Mpango huu tuhakikishe kwamba bandari hii inaanza mara moja kwa sababu kupitia bandari hii vijana wa Kigoma watapata ajira lakini sio Kigoma tu Tanzania nzima kwa sababu huu mpango ni wa Taifa watapata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyeiti, pia nimwambie Waziri kwamba mbali na ajira mzunguko wa pesa utakuwa ni mkubwa katika Mji wa Kigoma na mzunguko wa pesa ukiwa mkubwa katika Mji wa Kigoma hilo ni Taifa, Taifa tutapata pato. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri ufanye unavyoweza bandari hii ianze mara moja. Labda ningejua, Wizara ya Fedha mpaka sasa mmejipangaje katika suala hili na Mamlaka ya Bandari imefikia wapi katika utekelezaji wa maamuzi haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia Mpango wa Mheshimiwa Waziri. Hakuna mahali ambapo nimeona kuna uwezeshaji wa kijana na mwanamke. Hakuna mtu asiyejua kwamba kijana ni mtu muhimu katika Taifa hili lakini hakuna mtu asiyejua kwamba mwanamke ni mtu muhimu katika familia na Taifa. Naomba sasa Serikali ije na Mpango madhubuti wa kumwezesha kijana huyu ambaye leo anamaliza shule lakini hana ajira na mama huyu ambaye amekaa nyumbani hana kazi. Tuandae mikakati ambayo itamwezesha mama, wote tunajua mama ni nani katika familia, ukimwezesha mama atasomesha watoto. Kwa hiyo, tuwe na vyanzo vya kuwasaidia akina mama, mabenki yatoe mikopo kwa akina mama. Kwa hiyo, ningeomba Mheshimiwa Waziri katika Mpango unaokuja umfikirie sana kijana na mama wa Kitanzania, SACCOS za akina mama Serikali iweze kuzisaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tena suala la uwekezaji. Kumekuwa na maeneo mengi ambayo wawekezaji wanataka kwenda kuwekeza lakini hakuna ushirikiano mzuri. Kwa taarifa nilizozipata katika eneo hili hili la Kisezi, Mkoani Kigoma Serikali ya Japan inataka kuja kuwekeza, watengeneze bidhaa wao wenyewe na watafute masoko wao wenyewe masoko wao wenyewe na watumie uwanja wa ndege wa Kigoma. Hata hivyo, Serikali haioneshi ushirikiano na wawekezaji hawa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ningeomba kama kweli tunataka kusonga mbele katika maendeleo ya Taifa tutoe kipaumbele katika suala zima la uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika suala zima la kilimo. Hakuna mtu asiyejua kwamba kilimo ni uti wa mgongo. Wote hapa leo ni Mawaziri, Wabunge wengi tumesomeshwa na wazazi wetu kwa sababu ya kilimo. Naomba Mpango huu utakaokuja sasa muwasaidie wakulima, muwape pembejeo, mbolea, muwasaidie kupata masoko kwa sababu tunaposema leo tuna nchi ya viwanda, huwezi kuwa na viwanda kama wewe mwenyewe huna product za kupeleka kwenye kiwanda chako. Huwezi kusubiri mahindi kutoka Kenya, huwezi kusubiri korosho kutoka nchi jirani, tuhakikishe sisi wenyewe tunakuwa na product zetu ambazo tutazipeleka katika viwanda vyetu. Kwa hiyo, nimuombe sana Waziri, Wabunge wengi wameongelea kuhusu suala la kilimo, naomba kilimo kipewe kipaumbele, kilimo ni uti wa mgongo. Kama Serikali tunataka kusonga mbele tuhakikishe kilimo kinathaminiwa kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niongelee suala la elimu. Miundombinu ya elimu katika nchi yetu ni mibovu. Walimu wengi nyumba zao ni mbovu. Walimu hawa ndiyo wametufikisha mahali hapa leo. Walimu hawa ndiyo wamekutoa wewe Waziri, mimi Mbunge.

Kwa hiyo, naomba tuwathamini walimu kuanzia kwenye makazi, nyumba wanazokaa ni chache. Mikoa mingi ina changamoto walimu hawana nyumba na hata nyumba ambazo zipo unakuta haziko katika mazingira mazuri. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri atakapokuja na Mpango huu ahakikishe miundombinu kwa walimu, waongezewe mishahara lakini nyumba na makazi yawe mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika elimu nizungumzie suala la madarasa. Maeneo mengi hasa ya vijijini wanafunzi wanasomea nje, hakuna madarasa. Serikali ijitahidi kuweka madarasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nizungumzie miundombinu ya wanafunzi. Shule nyingi vijijini watoto hawana vyoo. Sasa jiulize kama tunashindwa kuweka matundu ya vyoo katika shule, binti huyu ambaye amekwenda shule, kwa sababu tayari kuna watoto wa darasa la saba wameshaanza kuona hali ya usichana wao, ameingia katika hali ya usichana hakuna maji, hakuna choo mnamweka katika mazingira gani binti huyu wa kike? Kwa hiyo, mnamfanya sasa huyu binti akishaingiwa na ile hali na wenzie wamemuona, kesho hawezi kurudi shule. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri mhakikishe mnawajali wanafunzi katika huduma za maji mashuleni, vyoo na hasa mtoto wa kike mumsaidie apate huduma hizi ili aweze kwenda shule kama watoto wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naomba kuunga mkono hoja, ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya leo. Nikiwa kama Mwanakamati wa Kamati ya Nishati na Madini, napenda kuipongeza Kamati ya Nishati na Madini kwa kazi nzuri ambayo wameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kuongelea suala la TANESCO. TANESCO ni taasisi ambayo tunaitegemea katika nchi yetu, lakini imeshindwa kufanya kazi yake ipasavyo kwa sababu ya haya madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la Kigoma. Mpaka leo mikoa hii ya Magharibi ambayo ni Katavi, Kigoma, tunatumia umeme wa dizeli ambao kwa namna moja ama nyingine unasababisha hasara kubwa kwa Serikali yetu. Sasa naiomba Serikali ijitahidi kadri inavyoweza, kwa sababu tayari wameanza mpango huu wa Gridi ya Taifa, basi mikoa hii ya Magharibi, Kigoma na Katavi tuweze kuingia katika Gridi ya Taifa haraka inavyowezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niongelee suala la wachimbaji wadogo wa madini. Wachimbaji wadogo wengi wa madini ni vijana wa Kitanzania ambao wengi wameamua kujishughulisha wasiingie katika wizi na wafanye kazi. Naiomba sasa Serikali iwasaidie vijana hawa, iwasaidie elimu, iwasaidie vifaa. Leo tumeona vijana wengi wamekuwa wakifunikwa na vifusi katika migodi kwa sababu hawana uelewa wanapoingia kule chini. Kwa hiyo, naiomba Serikali ijitahidi kadri inavyoweza itoe elimu kwa vijana hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine niongelee kuhusu REA. Naipongeza sana Serikali, pamoja na kufanya kazi vizuri katika REA II lakini kuna changamoto ambazo zimejitokeza. Naomba wanapokwenda katika REA III wajitahidi changamoto zile zisirudie. Kwa sababu tumeona vijiji vingine umeme unapita barabarani, lakini hauendi katika hospitali na shule. Umeme unakwenda Kijiji ‘A,’ lakini unaruka unakwenda Kijiji ‘C’, Kijiji ‘B’ kinakosa umeme. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, pamoja na kazi nzuri ambayo wanafanya katika Mradi huu wa REA, REA III iende vizuri na vijiji vyote vipate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la Chuo hiki cha Madini cha MRI. Tunahitaji wasomi ambao wamebobea katika suala zima la madini. Leo Tanzania tunatengeneza Tanzanite, lakini Tanzanite hii ambayo tukiipeleka katika Soko la Dunia ambayo imechachuliwa hapa Tanzania, inaonekana haina hadhi sawa na ile ya India au South Africa. Naiomba sasa Serikali iwasomeshe watu, iwapeleke nje, wakapate ujuzi ili kesho Tanzanite yetu hii ionekane sawa na ile ya India au ya South Africa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, Waswahili wanasema mnyonge, mnyongeni haki yake mpeni. Nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka ukuta huu Mererani ambao unalinda madini yetu ya Tanzanite yasiweze kuibiwa. Leo madini yetu hayataweza kuibiwa, yatatoka na yatapelekwa moja kwa moja kwa asilimia 100 na hakuna wezi ambao watapitisha tena haya madini kwa njia ya chocho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuniwezesha kuchangia leo hii kwa maandishi. Napenda kuanza kuchangia kwa kusema hakuna asiyefahamu kwamba kilimo ni uti wa mgongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yoyote duniani ambayo imefanikiwa, kilimo kinapewa kipaumbele kwa asilimia kubwa. Kilimo ndiyo tegemeo la wananchi wengi kwa asilimia 99. Wengi wetu tumefanikiwa hapa leo kwa ajili ya kilimo, wazazi wetu wanategema kilimo, maisha yao yanaongozwa na kilimo lakini leo kilimo hakithaminiwi kabisa kwani changamoto ni nyingi sana, wakulima wanapata shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima hawanufaiki kabisa na kilimo kutokana na kwamba mkulima analima, anatumia pesa na muda mwingi lakini anapovuna bei zinakuwa ndogo na hazimlipi kabisa ukilinganisha na gharama alizotumia. Leo Mkoa wa Kigoma wakulima wanalima kahawa, kwanza wanatumia gharama na muda mwingi ila anapokuja kuuza anauza kwa bei ndogo. Hii ni changamoto kubwa sana. Serikali iwasaidie sana wakulima kuuza mazao yao kwa bei nzuri lakini pia kuwatafutia masoko ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mbolea kutofika kwa wakati, mbolea zimekuwa zikichelewa, hazifiki kwa wakati. Wananchi wanateseka sana kwani mbolea zinafika mkulima anavuna. Hivi kweli hapa mnawasaidia wakulima au mnawakomesha? Leo wakulima wa korosho wanalia kwa kukosa sulphur kwa wakati. Niombe sana Serikali suala la mbolea liangaliwe kwa makini, wakulima imefika mahali wanakata tamaa katika mfumo mzima wa kilimo, wanaona bora wasilime lakini kilimo ndiyo tegemeo lao na msaada, wanategemea kusomesha watoto, kupata afya nzuri kupitia kilimo lakini wakulima wamepoteza matumaini kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viuatilifu vya kuua wadudu. Mazao mengi yanaharibiwa sana na wadudu kama viwavi jeshi, wakulima wanapata hasara kubwa sana. Mtu analima hekta 30 za mahindi lakini anapata hasara ya hekta 10, zinaharibiwa na wadudu. Naomba sana Serikali iwasaidie wakulima dawa za kuuwa wadudu. Watu wanajiua kwa kupoteza pesa, mtu analima hekta 50 anapata hasara kubwa, mazao hayazai, wadudu wanakula. Nchi za jirani zetu Barani Afrika mpaka sasa wametenga pesa kwa ajili ya kukabiliana na wadudu hawa waharibifu kama viwavi jeshi. Niombe sana Serikali itenge pesa sasa za kuhakikisha inawasaidia wakulima katika kupambana na wadudu waharibifu, wakulima wagawiwe dawa za kuulia wadudu na kuzuia. Hii itasaidia sana kupata mazao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migogoro ya ardhi na vyanzo vya maji, kumekuwa na migogoro mingi inayotokea katika maeneo mengi. Watu wanauana kwa kugombania ardhi. Niombe sana Serikali isimamie na kuwasaidia ardhi ya kutosha ili kuondoa maafa na migogoro ambayo inazidi siku hadi siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kigoma migogoro ya wakulima kugombania ardhi ni mingi sana katika vijiji vya Kasulu, Pamila, Manyovu na Kibondo. Wananchi wa Kasulu wanazuiwa kulima katika eneo la Kagerankanda wakati wananchi wamelima miaka mingi na ni eneo ambalo wanalitegemea na hata Mheshimiwa Rais alipopita aliwaahidi wananchi kutumia eneo lile lakini wanakuja viongozi wanatoa matamko yao na wanakwenda kinyume na kauli ya Rais. Niombe sana Serikali iwaachie wananchi hawa eneo hili waendelee kulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia kubwa ya wananchi wa Kigoma hasa Wilaya ya Kigoma Vijijini wanategemea zao la michikichi lakini zao hili limesahaulika kabisa na linaonekana kama halina thamani. Wenzetu wa Malaysia walikuja kuchukua mbegu kwetu, wamelipa thamani zao hili na sasa ni nchi inayosambaza mafuta duniani. Kwa hiyo, Tanzania tulifanye zao hili kama zao la biashara ukizingatia tunaenda katika nchi ya viwanda, kwa nini tusiwe watengenezaji wakubwa wa mafuta kwani katika michikichi tunapata mafuta mazuri sana kwa afya ya mawese, mise lakini pia kupitia mafuta haya tunapata sabuni nzuri sana za gwanjwi. Naomba Serikali iwapatie wananchi wa Kigoma mbegu bora za michikichi kwani kampuni inayouza miche hii inauza mche mmoja kwa shilingi 5,500, wananchi hawana uwezo wa kununua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kuiambia Serikali kilimo ndiyo kila kitu, wananchi wanategemea sana kilimo. Kama kweli tunataka nchi ya viwanda basi lazima Wizara ya Kilimo ipewe kipaumbele, bajeti iwekwe kubwa wananchi wamekata tamaa kabisa na kilimo.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia jioni ya leo, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na kuweza kusimama hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kabisa na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha Dkt, Philip Mpango pamoja na Naibu Waziri nimeipitia bajeti, niwapongeze sana kwa kuweza kupunguza kodi katika hizi taulo za kike. Naamini kwamba wamemfikiria binti wa Kitanzania ambaye yupo kijijini ambaye alishindwa kujiifadhi na wapo wengine mpaka kutumia majani kwa sababu ya kushindwa kupata hizi pads. Kwa hiyo, niwapongeze sana kwa kumfikiria binti huyu wa Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu suala zima la kilimo, wote tunafahamu kwamba kilimo ni uti wa mgongo. Wote tumefika hapa tulipo, wazazi wetu wamekuwa ni wakulima wamelima na leo Mheshimiwa Waziri wa Fedha umefika hapo naamini hata kule Buhigwe babu yangu alikuwa akilima na akamsomesha na amefika hapo. Ningeomba sana Mheshimiwa Waziri katika bajeti hii tuzingatie sana suala la kilimo, kwa sababu naamni kilimo ni uti wa mgongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri bado kuna mazao ambayo sijaona wakiyapa kipaumbele kwa mfano zao la mawese ndani ya Mkoa wangu wa Kigoma. Zao hili la michikichi, mbali na kwamba linatoa mafuta, pia linatoa bidhaa nyingi, tunaweza kutengeneza sabuni kwa kutumia michikichi, bado tunaweza kupata mafuta ambayo yanaweza yakalainisha ngozi na muonekano mzuri kwa akinamama, ningeomba sana tuweze kujali suala hili la michikichi na tutenge bajeti kwa wananchi wa Kigoma na maeneo mengine, tulifanye zao hili kwamba ni la biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika michikichi, leo michikichi iliyopo katika Mkoa wa Kigoma tayari imeanza kuzeeka, lakini wananchi wa Kigoma wako tayari kulifanya zao hili la biashara, naomba sana Mheshimiwa Waziri kuna mbegu bora ambazo sasa zinapatikana za michikichi waweze kuwagawia wananchi wazipate bure, mashamba yapo, maeneo yapo, waweze kulima na wapate mbegu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mche mmoja leo unauzwa kwa Sh.5,700, katika maisha ya kawaida mtu hawezi kulima heka moja na akaweza kupata michikichi hii. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie zao la michikichi Kigoma, Serikali iwagawie wananchi michikichi na tuko tayari kuweza kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tena zao la alizeti. Alizeti inalimwa katika maeneo ya Singida na maeneo mbalimbali. Ningeomba sana Serikali tulifanye hili kama zao la biashara, mikoa yote tuweze kulima alizeti tuweze kupata mafuta na tuweze kuondokana na uhaba wa mafuta katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie tena katika suala zima la afya, maeneo mengi ndani ya nchi yetu ya Tanzania bado kuna changamoto ya Wauguzi, hospitali nyingi hazina Wauguzi na hata nikitoa mfano katika Mkoa wangu wa Kigoma nimekuwa nikilisemea sana na kuuliza, kwamba hatuna Madaktari katika hospitali ya Mkoa, hata baadhi ya vituo havina Wauguzi. Unakuta kituo cha hospitali au zahanati kina Muuguzi mmoja katika hali ya kawaida bado tutaendelea kuwa na vifo vya mama na mtoto kwa sababu hatuna Wauguzi wa kutosha wa kutoa huduma kwa haraka na wakati unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri katika bajeti hii wanapokwenda kutenga fedha wahakikishe kwamba ajira hizi 8,000 wanazozitoa basi waweze kutusaidia ndani ya Mkoa wa Kigoma tupate Wauguzi wa kutosha na maeneo yote yenye changamoto hizi yaweze kupata Wauguzi. Wauguzi watakapokwenda katika maeneo husika basi waweze kulipwa pesa zao kwa haraka na kwa muda ambao unaostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie katika suala zima la ajira. Ajira imekuwa ni changamoto kubwa sana katika nchi yetu ya Tanzania hasa kwetu vijana. Vijana wengi wamekuwa wakimaliza vyuo; lakini wanakaa mtaani. Wao wanasema kwamba tujiajiri, kijana huyu wa Kitanzania anaweza kujiajiri vipi kama hata mtaji hana? Kwa hiyo, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika kuhakikisha kwamba wanaleta ajira kwa vijana hata kama wao wanajiajiri basi waweke mikakati ya kumwezesha kijana kujiajiri na biashara mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonesha kwamba sasa Afrika tunakabiliwa na tatizo la ajira, vijana wengi wamekuwa wakikimbilia nchi za ughaibuni kutafuta ajira, lakini katika bajeti hii sijaona Mheshimiwa Waziri ameelezea suala la ajira kwa vijana kwamba kama Waziri, kama Serikali wana mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wanawasaidia vijana wa Kitanzania na je, tupo katika hatari gani kama vijana wa Kitanzania kukimbilia katika nchi zingine kutafuta ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisikia watu wakiangukia katika bahari wanatokea Ethiopia, lakini hata Tanzania kuna vijana ambao wanakimbilia South Africa, wanaishi maisha magumu South Africa, wanateseka wanauawa, yote hiyo ni kwa sababu hakuna ajira, wanaona bora wakimbie nchi zingine kutafuta ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha baba yangu Dkt. Mpango waweke mikakati ya kumsaidia kijana wa Kitanzania kuondokana na changamoto ya ajira. Hii itasaidia vijana kujiepusha na vitendo vya wizi, lakini itawasaidia vijana hasa kina dada kuepukana na tabia hii ya kujiuza ili waweze kupata kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie tena katika suala la TRA. Tunasema kwamba ‘Hapa Ni Kazi Tu’ na kweli wananchi wanajituma kufanya kazi. Imekuwa inasikitisha hata Mama Lishe ambaye anajitahidi kuchuuza ili aweze kumsomesha mtoto na kuondokana na umaskini bado TRA wanamsumbua. Hata kijana huyu wa Kitanzania ambaye ametoka shule anasema ngoja nijiajiri nifungue kibanda changu niweze kupata riziki, bado TRA wanakimbizana nae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiukweli hii inakatisha tamaa na kwa stahili hii tutaendelea kuwa na vibaka na wezi ndani ya Taifa letu. Kwa hiyo, ningeomba sana TRA Mheshimiwa Waziri ukae nao uongee nao, imekuwa ni changamoto kubwa, imekuwa ni kero kubwa watu wanafunga maduka, imefikia hatua sasa mtu anaona nina milioni tatu siwezi kufanya biashara, kwa sababu milioni tatu hata dada akisema afungue kisaruni chake kidogo bado hataweza kufanikiwa kwa sababu TRA nao wako nyuma yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri suala zima la TRA kiukweli wakae nao chini waangalie ni jinsi gani wanaweza kutusaidia wananchi, isifike mahali sasa mtu unaogopa hata kufungua biashara yoyote kwa sababu unaamini TRA wanakwenda kunisumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie tena katika suala la nishati. Nipongeze sana Wizara ya Nishati kiukweli wanafanya kazi nzuri katika miradi hii ya REA maeneo mengi yamepata umeme na naamini hata yale ambayo hayajapata umeme yanakwenda kupata umeme katika REA III. Pia nipongeze mradi huu wa Mto Rufiji, binafsi naona ni mradi mzuri na naupongeza sana, lakini naomba kutia msisitizo kwamba tuhakikishe fedha zinakwenda kwa wakati, pia nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba tutenge bajeti ya kutosha katika suala zima la nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mradi huu pamoja na kwamba tunaenda kupata megawati nyingi za umeme lakini kwa sababu tunakwenda katika nchi ya viwanda bado naamini kwamba yawezekana ule umeme usitoshe na tukahitaji umeme mwingine, tuweze kuwa encourage hawa private sector investors waweze kuja kuwekeza na wenyewe katika nishati hii ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nishauri jambo moja, kwamba ingekuwa ni vizuri…..

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimalizie kwamba ingekua ni vizuri ikatengwa bajeti kwa sababu ya watu wa TANESCO wakafanya feasibility study and then ikaelezea kwamba hapa tunazalisha megawati kadhaa, tumetumia kiasi kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuweza kuchangia kwa maandishi siku hii ya leo. Pia niipongeze Wizara kwa jitihada inazozifanya lakini, pamoja na jitihada za Serikali bado katika nchi yetu kuna changamoto nyingi zifuatazo ambazo napenda kuiomba sana Serikali izifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maslahi ya Polisi, Polisi ni watu muhimu sana katika nchi yetu kwani ndiyo wanaotulinda raia na mali zetu, lakini kulinda hata amani ya nchi yetu, lakini polisi hawa hawana maslahi mazuri ya mishahara yao. Hii imekuwa ni changamoto kubwa sana kwa polisi kupelekea kuishi kwa shida, hii ni hatari kwani inaweza pelekea wao kuingia katika vitendo vya kiuhalifu kama unyang’anyi wa silaha, upokeaji wa rushwa ili wajiongezee kipato. Niiombe sana Serikali kuboresha mishahara ya Polisi kwa haraka, hii i tawaongezea munkari ya kufanya kazi kwa umakini zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba za Polisi, maeneo mengi ya nchi yetu makazi ya polisi kiukweli ni duni sana na hayaridhishi kabisa. Polisi wanaishi katika mabanda yaliyojengwa kwa mabati. Hii siyo sawa, polisi wapatiwe nyumba nzuri za kudumu na wao waishi kwa heshima. Leo Mkoani kwangu Kigoma polisi wanaishi katika nyumba duni sana humo humo baba, mama na familia hakuna usiri. Kiukweli hali si nzuri kabisa. Niiombe sana Serikali ijenge nyumba za kudumu na nzuri katika mikoa na wilaya zote nao polisi waishi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchakavu wa vituo vya polisi, vituo vingi vya polisi vina hali mbaya sana hasa mikoani. Unaweza jiuliza hiki ni kituo cha polisi au ni kitu gani? Kituo chakavu sana, hawa polisi nao ni binadamu wanahitaji kufanya kazi katika mazingira mazuri na hata raia wanaokwenda kupata huduma pale wahudumiwe katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio ya upoteaji wa watu, sasa hivi hali inatisha sana. Kumejitokeza matukio makubwa na ya kuhuzunisha sana, watu wanapotea na kuuawa mara kwa mara na watu ambao hawajulikani. Hali hii imezua taharuki sana kwa wananchi. Serikali niiombe sana kuhakikisha watu hawa wanaofanya vitendo hivi wanakamatwa kwa haraka na kuchukuliwa hatua kali mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, raia kubambikiziwa kesi na polisi. Baadhi ya polisi wamekuwa si waadilifu na kupelekea kulichafua Jeshi la Polisi kwani kumekuwa na malalamiko mengi sana toka kwa wananchi hasa vijijini. Wanabambikiziwa kesi na baadhi ya polisi wasio waadilifu kwa lengo la kujipatia pesa. Niiombe sana Serikali kuliangalia suala hili kwa jicho la pili kwani wananchi wengi wanateseka sana, mtu anapewa kesi kubwa wakati hahusiki. Hasa tuliopo mipakani kama Kigoma, wafugaji, wavuvi wamekuwa wakibambikiziwa sana kesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Polisi kujichukulia hatua dhidi ya raia wanapowakamata. Ninavyofahamu mimi kazi ya polisi ni kulinda raia na mali zake. Polisi anatakiwa kuhakikisha anamlinda raia asipate tatizo lolote lile hata anapomkamata amefanya kosa lolote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jukumu la polisi kumlinda mhalifu (raia) na kumfikisha kituoni akiwa salama pamoja na mali zake. Hata hivyo, polisi wamekuwa wanaua raia kwa kuwapiga mpaka kupoteza maisha. Hii ni hatari sana sana kupita maelezo. Hata kama raia amekosea ni jukumu la polisi kumlinda na kuhakikisha anafika kituoni salama. Tumeona Musoma Polisi kamchoma kisu raia, kweli polisi wanafikia huku? Hii ni hatari kubwa na inasikitisha sana. Niiombe Serikali hii sikivu polisi hawa wachukuliwe hatua kali mara moja iwe fundisho kwa wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto kubwa sana katika Jeshi la Zima Moto, maeneo ya Wilayani hakuna vifaa vya zima moto vipo mikoani tu. Hii ni hatari sana lakini hata maeneo ambayo yanazima moto bado changamoto ni kubwa, vifaa wanavyotumia kwani inategemea ukubwa wa moto. Niombe sana Serikali iweke vikosi hivi vya zima moto katika maeneo yote ya Wilayani na mijini pia, majengo yawepo ya kutosha. Niombe sana Serikali ijenge majengo ya kutosha, vifaa vya zimamoto vya kutosha katika maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhamiaji maeneo mengi hayana ofisi. Niombe Serikali ijenge ofisi za uhamiaji za kisasa hasa katika Mikoa iliyopo mpakani kama Kigoma, Kagera, Tunduma, lakini utoaji passport umekuwa wa shida sana na bei ya kupata passport ni kubwa kwa raia.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika ripoti hii ya Kamati. Kwanza kabisa, nianze kwa kumpongeza Waziri wa Nishati pamoja na Waziri wa Madini kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze katika suala la REA, bado kumekuwa na changamoto kubwa Mheshimiwa Waziri katika suala la REA III. Vijiji vingi katika maeneo mengi bado umeme haujafika. Kwa mfano tu, katika Mkoa wangu wa Kigoma kuna Vijiji kwa mfano Msimba na Kamara umeme umepita katika eneo moja lakini eneo lingine umeme haujafika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vijiji kwa mfano, Kamanyangwe, Kihinga, Kalongolonge na Kingungo, bado hawajapata umeme lakini umeme umepita barabarani. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri pamoja na kazi nzuri ambayo mnaifanya, lakini mhakikishe kwamba vijiji vyote vinaweza kupata umeme huu wa REA III. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee tena suala la gridi ya Taifa. Sote tunajua kwamba Mikoa ya Kigoma na Katavi mpaka sasa hatujaingia katika gridi ya Taifa. Tunatumia umeme huu wa Diesel TANESCO ambao ni gharama kubwa na kusababishia Serikali yetu hasara kubwa. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, kwa sababu tayari mmeanza sasa mchakato, basi hiyo Februari, 2020 gridi ya Taifa iweze kukamilika katika Mikoa hii ya magharibi, Kigoma na Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie tena suala la mradi wa Mto Malagarasi. Nniseme kwamba wananchi wa Kigoma tumeupokea vizuri mradi huu na tunaunga mkono juhudi za Serikali kwa kuanzisha mradi huu wa Malagarasi Megawati 45 kutoka Malagarasi kwenda Kidahwe. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri pesa ziende kwa wakati, Wakandarasi wamalize kazi kwa wakati. Wananchi ambao wamepisha mradi huu, waweze kupewa fidia zao kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilimwuliza Mheshimiwa Waziri kwenye Kamati akaniambia tayari wameanza kuthaminisha. Naomba sana wananchi hawa kwa sababu wamejitoa na kupisha mradi huu waweze kupatiwa fidia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie katika suala madini. Wachimbaji hawa wadogo wa madini, wengi ni vijana wa Kitanzania ambao wameamua kujiajiri kwa kufanya kazi, lakini bado wamekuwa na changamoto kubwa, kwamba kwanza hawana elimu ya kutosha, lakini hawana vifaa na hata pesa hawana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, kaka yangu, Mheshimiwa Doto awaangalie hawa wachimbaji wadogo kwa jicho la pili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na tozo nyingi sana za ushuru. Tumeona hapa katika ukurasa wa 22 wa Kamati, kuna VAT asilimia 18, withholding tax 5%, service levy 0.3, inspection 1% na mrahaba wa madini ghafi ya vito 6%. Michango hii imekuwa ni mingi. Tozo zimekuwa nyingi kwa hawa wachimbaji wadogo wadogo. Kwa hiyo, kama tozo zitakuwa ni nyingi bado hatutaweza kuepuka tatizo hili la wachimbaji kutorosha madini. Naomba Serikali iangalie iweze kupunguza hizi tozo kwa wachimbaji wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukiona kwamba wachimbaji hawa wadogo wadogo mara kwa mara vifo vimekuwa vikitokea katika maeneo yao. Najua ni kwa sababu hawana uelewa wa kazi ambayo wanaifanya. Naiomba sana Wizara itoe elimu ya kutosha kwa wachimbaji wadogo wadogo ili waweze kuondokana na madhara haya ya vifo ambayo wamekuwa wakipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, nizungumzie suala la GST. Hawa wanajiolojia ni watu muhimu sana ambao wanaweza kutusaidia kutambua madini mbalimbali katika maeneo mbalimbali, lakini wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kukosa bajeti na fedha za kutosha. Naiomba sana Serikali iwapatie watu hawa pesa waweze kuzunguka katika maeneo mbalimbali, waweze kutuambia ni madini gani yanapatikana katika maeneo hayo hususan ukiwepo Mkoa wangu wa Kigoma ambao naamini kuna madini ya chokaa na hata dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hotuba hii ya TAMISEMI na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya nimeweza kusimama jioni hii ya leo. Kwa kipekee kabisa nimpongeze Fulbright Prof. Ibrahim Haruna Lipumba kwa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia hotuba hizi za Wizara hizi mbili, natambua Serikali inapambana kuhakikisha inaleta huduma bora kwa wananchi. Kwanza nianze na suala la TARURA. Barabara za vijijini ni muhimu sana katika maeneo yetu. Wote tunafahamu kwamba wakulima wote wako vijijini lakini barabara hizi ndizo ambazo zinaweza kuwasaidia kutoa mazao mashambani na kuleta mijini kutafuta masoko lakini hali ya barabara hizi kiukweli ni changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi kubwa ambayo TARURA wanaifanya, moja ya changamoto ambayo inawakabili ni suala zima la bajeti. Niiombe Serikali katika bajeti hii tunayokwenda nayo tuweze kuwasaidia TARURA wapate bajeti ya kutosha ili waweze kufanya kazi yao na kumaliza miradi hii ya barabara zetu huko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la bajeti tumeona TARURA wanapata asilimia 30 na TANROADS wanapata asilimia 70. Naelewa Serikali mmeunda Kamati Maalum kwa ajili ya suala hili na mimi nichangie na kuiomba Serikali kwamba at least sasa TARURA wabaki na 40 na TANROADS wapewe 60 kwa sababu ya barabara za viwango vya lami na madaraja kama ya Mfugale. Kwa hiyo, tuwasaidie watu wa TARURA, naamini wanafanya kazi na kama watapata bajeti ambayo inatosha wataweza kutusaidia barabara zetu hizi kumalizika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kwenye TARURA changamoto nyingine ni vitendeakazi, watu hawa hawana magari ya kuweza kutoka sehemu moja na kwenda site. Mfano Mkoa wangu wa Kigoma takribani wilaya zote, kuanzia Kigoma DC, Buhigwe, Kasulu, watu wa TARURA hawana magari na imekuwa ni usumbufu mkubwa katika utendaji wao wa kazi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri muangalie ni jinsi gani Kigoma wilaya zote tunaweza tukapata magari kwa watu hawa wa TARURA ili wafanye kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze katika suala la afya. Natambua Serikali mnajituma na mnafanya kazi kuhakikisha mnaboresha vituo vya afya na kutuletea wauguzi. Niwashukuru kwamba Kigoma mwaka jana tuliomba, mmetuletea Kigoma nzima watumishi 402 lakini kiukweli bado changamoto ni kubwa. Maeneo mengi ukienda hospitali za Kigoma na hata maeneo mengine ya Tanzania bado hatuna wauguzi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka kufikia Novemba, 2018 Kigoma tulikuwa na wafanyakazi 2,004, kiukweli bado idadi ya wafanyakazi ni ndogo ukizingatia Kigoma tuko zaidi ya watu milioni mbili lakini ni mkoa ambao tuko mpakani tunahudumia mpaka wakimbizi kutoka Kongo na Burundi. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali, pamoja na jitihada ambazo mnafanya lakini mtuangalie kwa jicho la pili mtuongezee wauguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo katika afya, Kigoma tuna Hospitali hii ya Mkoa ambayo inaitwa Maweni. Mpaka sasa hatuna vifaa kama CT Scan na x-ray machines za kutosha hali inayosababisha usumbufu mkubwa sana kwa wananchi watu wanakwenda kutibiwa pale wanahitaji huduma hii ya CT Scan wanapewa rufaa kwenda Mwanza (Bugando) au kwenda Muhimbili. Kulingana na hali ya maisha ilivyo, siyo watu wote wataweza kwenda Muhimbili au Bugando kwa wakati. Sasa kama tunataka kuwasaidia wananchi ili tupunguze vifo, niombe sana Serikali muweze kutusaidia vifaa hivi vya CT Scan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado niko katika hospitali ya mkoa; hospitali hii kama nilivyosema inahudumia watu wengi sana lakini mpaka sasa hatuna ma-specialist wa kutosha, tuna specialist mmoja wa akina mama na mmoja wa watoto. Kuna magonjwa mengine kama haya ya kisukari hatuna ma-specialist. Niombe sana Serikali mtusaidie hospitali hii tuweze kupata ma-specialist wa kutosha, mtakuwa mmetusaidia watu wa Kigoma na maeneo mengine Tanzania ambayo hakuna ma-specialist katika hospitali zao muweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie tena suala la miundombinu hospitalini na kwenye shule zetu. Sote tunajua kwamba walimu, madaktari na wauguzi ni watu muhimu sana katika maisha yetu, lakini watu hawa wamekuwa wakiishi maisha magumu kwa maana ya kwamba hata nyumba bora za kukaa hawana. Niombe sana Wizara muweze kuangalia suala hilo, muwajengee nyumba wauguzi na walimu ili nao waweze kukaa katika mazingira bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili la moboma, kuna majengo ambayo wananchi wamejitoa, niseme tu kwamba wananchi wanaunga mkono Serikali kwa kufanya vitu mbalimbali kama ujenzi wa zahanati, kujenga shule na hostels za wanafunzi lakini inafika muda na wao wanakwama. Niombe sana Serikali muwasaidie wananchi muweze kumalizia majengo haya ambayo yameishia kwenye lenta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano tu katika Mkoa wangu wa Kigoma, Awamu ya Nne Rais aliyepita aliahidi kujenga hospitali katika eneo la Nyarubanda na Mahembe na wananchi waliitikia wakaanza kujenga lakini sasa imesimama na hakuna mwendelezo wowote. Niombe sana Serikali muwasaidie watu hawa waweze kumalizia majengo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la vitambulisho. Niseme tu kwamba mimi ni mdau wa maendeleo na naunga mkono jitihada za Serikali katika ukusanyaji wa kodi lakini tuwe wakweli; pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais alisema hawa wajasiriamali wadogo wakate vitambulisho lakini tuwaangalie hawa wajasiriamali wadogo ni wa aina gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo katika Mkoa wangu wa Kigoma, mimi natokea Kijiji cha Mwandiga, baada ya Bunge kuisha kuna akina mama nilikwenda kuwatembelea sokoni. Kuna mama ambaye anauza ndizi kwa sababu tu nyumbani kwake amepanda ndizi, anaona ndizi zimeiva anasema nipeleke sokoni nikapange chini ili wanangu waweze kupata daftari na kupata mafuta ya taa. Sasa hawa ambao wanakwenda kutoa vitambulisho hivi unakwenda kumtoza mama kama huyu Sh.20,000 anaitoa wapi wakati biashara anayofanya haikutani mzunguko wake kupata Sh.20,000? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kiukweli malalamiko ni mengi. Kama tunasema ni Serikali ya wanyonge, wanyonge ndiyo hawa akina mama na vijana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na uzima na kuweza kuchangia leo hii katika hotuba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara hii kwa jitihada ambazo zimekuwa zikifanyika katika kuhakikisha ulinzi na usalama unaimarika katika nchi yetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Kangi Lugola na Naibu wake kwa kazi wanazozifanya.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada zinazofanywa na Wizara hii lakini bado kuna changamoto katika mipaka yetu. Mimi natokea Mkoa wa Kigoma, huu ni mkoa ambao tunapakana na nchi nne za Congo, Burundi, Zambia na Rwanda ambapo mwingiliano na wenzetu hawa ni mkubwa.

Mheshimiwa Spika, mipaka yetu haina ulinzi wa kutosha kwani wakimbizi hawa wamekuwa wakifanya matukio ya kihalifu. Tumeona matukio ya ujambazi yakishamiri kila kukicha kwa kutumia silaha za moto, wananchi wamekuwa na hofu hawana amani na maisha yao. Hivyo niiombe sana Serikali tupate askari wa kutosha katika Wilaya zote za Kasulu, Kibondo, Buhigwa, Kigoma na Mkoa wetu kwa ujumla watu wake waishi kwa amani pasipo hofu ya ujambazi huu.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie tena suala la hawa ndugu zetu askari. Hawa ni ndugu zetu lakini ni watu muhimu sana kwani hawalali wakilinda usalama wa raia na mali zao, lakini pia amani ya nchi yetu. Niombe sana Wizara iwaangalie hawa askari wetu kwa jicho la pili kwani wanaishi katika mazingira magumu sana, hawana makazi bora na imara, wengi wanaishi mpaka kwenye nyumba za mabati, hii si sawa. Naomba sana Wizara iwathamini wapate nyumba za kutosha bora na imara, hii itawasaidia hata kuongeza bidii katika kazi. Pia watu hawa wamekuwa wakifanya kazi muda mrefu bila kupandishwa vyeo, niombe sana tuwalipe fadhila wapande vyeo kwani wanafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Spika, niguse suala la Vitambulisho vya Taifa. Kiukweli bado wananchi wengi sana hawajapata hivi vitambulisho, leo watu milioni 16 ndiyo ambao wamepata vitambulisho hivi wakati Tanzania ina watu zaidi ya milioni 50. Niombe sana Serikali iongeze kasi kuhakikisha wananchi wote wanapata vitambulisho na tumeona Wizara ya Uchukuzi na Mawasiliano wanasema kuanzia mwezi ujao watu watasajili line kwa kutumia Vitambulisho hivi vya Taifa. Niseme hili zoezi lisitishwe kwanza mpaka pale wananchi wote watakapopata hivi vitambulisho kama kweli tuna nia ya kuwasaidia hawa wananchi.

Mheshimiwa Spika, nigusie suala la ujenzi wa vituo vya polisi. Kiukweli hali ni mbaya sana yaani kuna vijiji ukifika unaweza lia kwa huruma, kwani majengo yao yapo katika hali mbaya sana. Unajiuliza hii ofisi kweli ndiyo wanafanyia kazi hawa askari wetu wanaolala usiku kucha wakilinda mipaka, usalama wa raia na mali, ofisi inataka kuanguka, hakuna hata vitendea kazi, kiukweli hii siyo sawa.

Mheshimiwa Spika, leo katika Kijiji cha Mwindiga ninapotoka kituo cha polisi kina hali mbaya sana, kituo kidogo lakini hakuna hata vitendea kazi, hawana magari. Naomba sana Wizara mkarabati vituo vya polisi lakini magari ya kutosha yapelekwe katika maeneo mengi kwani hali ni mbaya.

Mheshimiwa Spika, kwa leo niishie hapa, nashukuru kwa kuweza kupata muda wa kuchangia leo kwa maandishi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na uzima na kuweza kuchangia katika Wizara hii kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri mama yangu Mheshimiwa Prof. Ndalichako kwa jitihada ambazo amekuwa akizifanya katika kuboresha suala la elimu Tanzania. Pamoja na jitihada zinazofanywa na Wizara bado kuna changamoto nyingi katika suala la elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu. Asilimia 90 ya wanaoomba mkopo wazazi wao hawana uwezo lakini pamoja na Serikali kuboresha huduma hii, bado kuna changamoto kwani wapo wanafunzi ambao wana vigezo kabisa vya kupata mkopo lakini hawajapata. Naomba sana Wizara ihakikishe wanafunzi wote wanapata mkopo na kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inasema inasaidia wanafunzi wasio na uwezo kupata mkopo, sawa tunashukuru sana kwa jambo hili jema linalofanya na Serikali yetu lakini kwa nini Serikali iwasaidie wanafunzi hawa kwa riba? Leo Serikali inampa mwanafunzi mkopo Sh.7,000,000, lakini anakuja kulipa Sh.12,000,000. Sasa huu ni msaada kweli ukizingatia anamaliza chuo anaanza kazi mshahara ni mdogo na hata kupata hiyo kazi ni shida. Kwa nini mwanafunzi asilipe kile ambacho Serikali imempa? Kama digrii amesoma miaka mitatu kwa Sh.8,000,000 basi akianza kulipa alipe hiyo hiyo na siyo Sh.13,000,000 au Sh.14,000,000. Hii sidhani kama ni sawa na kiukweli inaumiza sana. Naomba mtu alipe alichokopeshwa na siyo na riba tena kubwa inakuwa kama umekopa benki, hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala upungufu wa walimu hasa masomo ya sayansi. Shule zetu nyingi hazina walimu wa kutosha wa sayansi. Sasa kama kweli tunaenda katika nchi ya viwanda ni lazima tuwekeze katika suala la sayansi katika shule zetu. Niombe sana zijengwe maabara za kutosha ili wanafunzi wetu waweze kufanya mafunzo kwa vitendo, hii itawasaidia sana kwani sayansi ni vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la miundombinu kwenye shule zetu kiukweli kuna changamoto kubwa kwani maeneo mengi hakuna madarasa ya kutosha. Katika Mkoa wangu wa Kigoma hakuna madarasa ya kutosha kwani kuna shule wanafunzi wanakaa chini. Vilevile shule nyingi hakuna vyoo bora yaani hali ni mbaya sana, watoto wana mazingira magumu sana. Unakuta watoto wanajisaidia hovyo na kupelekea mlipuko wa magonjwa kama kipindupindu. Pia kuna watu wenye ulemavu wanaotambaa chini sasa angalia hali ya choo ilivyo chafu na hakuna maji hawa wanafunzi wanakuwa katika hali gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba bora kwa walimu. Walimu ni muhimu sana, tuwe wakweli wote tumefika hapa kwa msaada wa walimu. Walimu wanafanya kazi kubwa sana lakini wanaishi katika mazingira magumu sana. Wengi hawana nyumba za kuishi na hata zilizopo zina hali mbaya sana kwani hakuna maji wala vyoo bora. Naomba Serikali iwaangalie walimu Tanzania nzima kwa jicho la pili wapatie nyumba bora za kuishi. Hii itasaidia kuongeza morale ya utendaji kazi wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la kupanda madaraja kwa walimu na stahiki zao za likizo na matibabu. Bado kuna changamoto kwani walimu wanapanda madaraja lakini mshahara haupandi, anapanda daraja toka A kwenda B, lakini anaendelea kulipwa mshahara wa daraja A. Hali hii imepelekea mpaka leo kuna wastaafu wamestaafu lakini wamepunjwa mafao yao kwa kufanyiwa kikokotoo kwa mshahara wa daraja A wakati alipanda daraja miaka mingi na amestaafia daraja jipya. Jambo hili si haki kabisa, huyu mtu ametumikia Serikali kwa moyo wote kwa nini anyimwe haki yake? Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya maji. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima na afya na kuweza kusimama mchana huu wa leo. Kipekee kabisa niungane na wewe katika kuwapa pole Watanzania na wanafamilia wote kwa kuondokewa na mzee wetu, Mzee Mengi na Mungu amlaze mahali pema Peponi, amen.

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri Naibu Waziri, na jopo lote la maji kwa kazi ambayo wamekuwa wakiifanya katika kuwasaidia wananchi suala la maji. Ni ukweli usiopingika kwamba changamoto ya maji bado ni kubwa katika maeneo mengi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nizungumzie suala la Kigoma, kwa sababu tunasema charity begins at home. Sasa nami nianze kuwapigania wananchi wa Kigoma ingawa changamoto ya maji ni Tanzania nzima.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ambayo natokea ya Kigoma DC, tuna miradi miwili ya maji; tuna Mkongolo I, tuna Mkongolo II. Miradi hii imeachwa, imetelekezwa, miundombinu ni mibovu. Pia miradi hii inahudumia zaidi ya watu 50,000 Vijiji vya Mwandiga, Bitale, Mkongolo, Nkungwe, Kiganza na maeneo mengine ya Kigoma DC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa namwomba sana Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Kigoma tunateseka, hatuna maji. Leo nimefikisha miaka 30, lakini mama zangu wanabeba maji kuanzia sijazaliwa mpaka sasa. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri wasaidieni wamama wa Kigoma. Kama kweli tunasema ni Serikali ya wanyonge, kama kweli tunataka kumtua mama ndoo kichwani, tuwasaidie akina mama ambao nywele zimeisha katikati kwa sababu ya kubeba ya ndoo ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi natokea Kijiji cha Mwandiga. Hapo Mwandiga kuna Mzee mmoja anaitwa Mzee Sheni, ni Mhindi. Huyu amechimba kisima, anawasaidia watu hawa wa hapo, ndoo shilingi 100/=. Sasa leo tunaposema kwamba mtu kama huyu atoe tozo kwa sababu ya kuchimba kisima, sidhani kama tunamtendea haki. Kwanza amewasaidia wananchi, ambao kwa miaka zaidi ya 30 tunatumia maji ambayo siyo safi na salama. Mwandiga tumekuwa ni kinara wa ugongwa wa kipindupindu kwa sababu hatuna maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naungana na Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba tozo hii kwa sababu ya kuchimba visima, iweze kuondolewa. Kaka yangu, Mheshimiwa Nape alielezea vizuri kwamba hawa ambao wanauza maji labda haya ya kunywa ambayo wanafunga kwenye makatoni, sawa; lakini hawa ambao wanachimba visima kwa sababu ya kuwasaidia wananchi, kama tutawatoza tozo, kiukweli hatuwatendei haki. Kwanza wanawasaidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, yuko mwingine amechimba nyumbani kwake kwa sababu ya matumizi yake binafsi. Haiingii akilini tunapomwambia atoe shilingi 700,000/=, atoe kiasi cha fedha kwa sababu ya kuchimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongezee suala lingine katika Mkoa wa Kigoma. Nashukuru katika Kitabu cha Mheshimiwa Waziri amesema kuna mradi wa Ziwa Tanganyika Naomba sana huu mradi utekelezwe na ukamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kuna maji ambayo yako katika Manispaa ya Kigoma Mjini kwa kaka yangu Mheshimiwa Zitto, lakini haya maji yanakuja yanaishia katika mpaka wa Mwandiga na Kigoma Mjini ambako panaitwa Ntovye. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, haya maji ambayo yanaishia pale yasiweze kupotea yapande katika Kijiji cha Mwandiga, yapande katika Kijiji cha Bitale na Kijiji cha Kiganza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mwaka 2018 nakumbuka niliuliza swali kwamba Serikali ina mkakati gani wa kuleta maji ya Kigoma Mjini yapande mpaka Vijiji vya Mwandiga na kuendelea? Kaka yangu Mheshimiwa Aweso alinijibu akaniambia kwamba wapo kwenye mkakati. Nafahamu juhudi ambazo zinafanywa, sasa nawaomba sana wasichelewe, tusaidieni wamama wa Mwandiga na maeneo mengine tuweze kuondokana na changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Nizungumzie suala lingine. Ndani ya Halmashauri ya Kigoma DC kuna vijiji ambavyo mpaka sasa kwenye miradi tunatumia dizeli na mafuta, kitu ambacho tunasababisha hasara kwa Serikali yetu kutokana na gharama ambayo tunaitumia. Sasa katika Vijiji kwa mfano, mradi katika Kijiji Nkungwe, Kalinzi kule kwetu na Kandanga tunatumia dizeli na umeme, ni gharama kubwa. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri kama tungepata solar naamini ingeweza kutusaidia na wakafanya kazi kwa ufanisi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisisitize, mbali na kwamba nimeongelea Kigoma, lakini bado kuna maeneo mengine hata Dar es Salaam, suala la maji ni changamoto, kwa mfano, Goba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakazi wa Goba, wamekuwa wakiteseka, hakuna maji ya uhakika na ninatambua kuna mradi pale unaendelea. Sasa huu mradi ambao umekuja umeishia Kinzudi. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri huu mradi uweze kusambaa katika eneo lote la Goba, wakazi wa Goba waweze kupata maji safi na salama, lakini tuondokane na kero ambayo wakazi wa Goba wamekuwa wakiipata kwa kukosa maji kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine nizungumzie changamoto ya watumishi; Kigoma suala la maji katika Idara ya Maji bado tuna changamoto ya watumishi. Niombe sanawatusaidie watumishi waongeze nguvu katika halmashauri zetu tupate Wahandisi wakutosha. Kipekee kabisa Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni na kama mtu anafanyakazi apongezwe, nampongeza Mheshimiwa Waziri, baba yangu Mbarawa anafanyakazi. Sasa naomba Mhandisi Mkoa wa Kigoma nikijana kama mimi, anafanyakazi kwa kujituma, naomba tumuunge mkono mpaka sasa bado anakaimu, lakini amekuwa ni kinara katika kushirikiana na wananchi wa Kigoma kutatua kero mbalimbali za maji. Sasa kama anatusaidia wananchi wa Kigoma na anafanya kazi vizuri, basi Mheshimiwa Spika kipekee kabisa naomba huyu kijana aweze kupewa haki yake na asibaki kukaimu kwa muda mrefu.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiendelea kuongea nafikiri nitakuwa narudia ambayo wenzangu wameshaongea, naomba sana Mheshimiwa Waziri haya ambayo nimemwomba Mji wa Mwandiga tupate maji, lakini vijiji vingine ambavyo havijawahi kuona maji kabisa kwa mfano Kiziba, Kalalangabo naMatyazo hawajawahi kuona maji kwenye mabomba wala maji safi na salama. Naomba sana Mheshimiwa Waziri uweze kuwasaidia watu hao wapate maji na waone faida ya kuwa na Ziwa Tanganyika katika mkoa wao.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niseme nakushukuru.(Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima na afya na kuweza kuchangia katika bajeti hii muhimu ya Serikali. Naomba nianze na kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha Dkt. Mpango pamoja na Naibu Waziri wake Dkt. Kijaji kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeisikia bajeti lakini nimepata fursa ya kuisoma. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na jopo lake kwa kuyafanyia kazi baadhi ya mambo. Niwapongeze sana kwanza kwa kuondoa tozo ya uchenjuaji madini, kwa hili niseme Mheshimiwa Waziri umesaidia sana sekta ya madini kwani kwa uchenjuaji kufanyika hapa hapa nchini kwetu itasaidia sana kuleta ajira hapa hapa nchini, tofauti na awali ambapo madini kama ya Tanzanite yalikuwa yakipelekwa nje kama India kwa ajili ya uchenjuaji ambapo tulikuwa tukipoteza ajira lakini fursa nyingi kwa nchi yetu. Pamoja na mazuri haya ya kuondoa tozo mbalimbali ikiwemo tozo ya kila mwezi ya visima (maji) bado kuna mambo ningependa kumshauri Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la taulo za kike (pads). Kama kuna jambo Mheshimiwa Waziri naomba nichukulie na kukuomba leo basi ni suala la VAT katika taulo hizi za kike. Mimi ni mtoto wa kike naelewa changamoto zinazopatikana katika kipindi cha hedhi. Mimi nakaa na wanafunzi wa kike, naona, najua shida wanayoipata pindi tu wanapoingia katika siku zao. Mtoto huyu wa kike kila mwezi anapoteza takribani wiki nzima ya kutuingia darasani kutokana na kushindwa kwenda shule kwa kuwa tu anaohofia kuchafuka na kuonekana awapo shuleni na ni kwa sababu tu hana taulo ya uhakika ya kujihifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, taulo hizi za kike ziweze kuingizwa bila VAT ili kurahisisha upatikanaji wa taulo hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko vijijini hali ni mbaya, watoto wa kike kuna maeneo ambayo wanatumia mpaka majani kutokana na uwezo wao kuwa duni, maisha ya wananchi ni masikini, mzazi hawezi kununua pads hizi kwa bei iliyopo. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri acha kumbukumbu kwa watoto wa kike katika uongozi wako, wasaidieni taulo hizi zipatikane kwa urahisi; hivyo hakuna budi kuondoa VAT ili taulo hizi zipatikane kwa wingi vijijini na mijini na utakuwa umemsaidia sana mtoto wa kike aliyepo hata kule kwetu Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la uwekezaji katika nchi zetu zilizoendelea. Suala la uwekezaji ni muhimu sana sana. Sasa Mheshimiwa Waziri niombe Serikali yetu ipeleke pesa katika uwekezaji wote uliofanyika nchini. Kwa wakati miradi ya umeme wa Mto Rufiji Mradi wa Standard Gauge na bandari zote, kwa miradi hii kukamilika tutaweza kupiga hatua kama nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la uwekezaji niombe sana Mheshimiwa Waziri, ni lazima watu wa TRA watengeneze mazingira mazuri na wafanyabiashara ni lazima tuwakaribishe na kuwapa fursa wawekezaji binafsi.

Tumeona wananchi wakilalamikia hali ya biashara kuwa ngumu na tuhuma zikienda kwa TRA; hata namna ya ukusanyaji kodi na hasa wafanyabiashara wengine wamefikia kufunga biashara. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri kwa hali yoyote ile Serikali yetu ihakikishe tuna encourage wawekezaji kwani kwa kufanya hivyo tutaongeza ajira za kutosha na mapato pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie suala la malipo. Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango wafanyakazi hasa walimu wamekuwa wakicheleweshewa malipo mbalimbali. Niombe sana malipo kwa wafanyakazi yaweze kufanyika kwa wakati na madeni wanayodai Serikali basi waweze kupatiwa kwa wakati ahsante.