Contributions by Hon. Salma Rashid Kikwete (21 total)
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima na uhai. Kabla sijaanza naomba niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Kwa kweli Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli imefanya mambo mengi na makubwa katika nyanja mbalimbali. Kila eneo kwa kweli imefanya kazi kubwa na ni kazi ambayo kwa kipindi kifupi imeweza kuonekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi za pekee vilevile zimfikie Mheshimiwa Mama Samia Suluhu, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa ambaye yeye ndiye Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni. Shukrani nyingine za pekee ziwafikie Waheshimiwa Mawaziri wote ambao wako kwenye Serikali hii ya Awamu ya Tano, hongereni sana kwa kazi nzuri na kubwa ambazo mnazifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nizungumzie maeneo makubwa mawili; kwanza nizungumzie afya ya mama na mtoto pamoja na eneo la UKIMWI kwa ujumla wake. Kabla sijaenda kwenye maeneo hayo, niseme kwamba Serikali hii ina dhamira ya makusudi kabisa ya kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wanaishi kwa kuwa na afya bora na nzuri zaidi na ndiyo maana kwa misingi hiyo hata ukiiangalia bajeti ya mwaka 2016/2017 inatofautiana sana na bajeti ya mwaka 2017/2018. Hii ni kuuthibitishia umma kwamba Rais, Mheshimiwa Magufuli ana dhamira ya dhati kuwaweka Watanzania kwenye afya nzuri na afya bora zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie afya ya mama na mtoto. Takwimu zinaonesha kwamba katika vizazi hai 100,000 wanawake 556 hufariki dunia. Wanawake hawa 556 ambao wanafariki dunia hii takwimu ni kubwa zaidi. Hatutaki mwanamke hata mmoja afariki wakati analeta kiumbe kingine. Kwa kweli kwa misingi hiyo hili jambo ni lazima litazamwe kwa jicho la pekee kabisa ndani ya Wizara hii. Nasema haya kwa sababu kubwa za msingi. Sababu ya kwanza, takwimu hizi kwa mara ya mwisho zilikuwa 446 hivi lakini sasa zimetoka kwenye 446 zimefika kwenye 556, hapa ni lazima tupaangalie kwa namna ya pekee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiachana na vizazi hai, tunaingia kwenye eneo la watoto, watoto 25 kati ya 1,000 wanapoteza maisha. Watoto hawa wanaopoteza maisha lengo letu ndiyo waje kuwa watu wazima hatimaye washike mamlaka ndani ya Taifa lao. Sasa kama hivi leo tunawapoteza watoto hawa nini matokeo ya baadaye? Hili jambo ni lazima liwe kwa mapana yake kama ambavyo tumeangalia katika maeneo mengine tusiruhusu mtoto afe wakati akija duniani. Naiomba Serikali/Wizara ihakikishe kwamba wanaboresha maeneo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine, akina mama waliambiwa waende na vifungashio hospitalini. Leo hii akina mama wanabeba vifungashio vyao na akina mama hawa ni maskini, tunafanyaje juu ya jambo hili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, narudia tena kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, hatimaye nikushukuru wewe kwa kuniona na kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye Wizara ya Maji na Umwagiliaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawapongeza sana Mawaziri wa Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Sambamba na hilo, naomba niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya. Kikubwa zaidi, niipongeze Serikali kwa kipaumbele ambacho imeweka kwenye Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, naomba niwape pole Watanzania wote kwa matatizo ambayo yametokea nchini kwetu na siyo matatizo mengine bali ni matatizo haya ya mvua ambayo ipo kila kona na yameweza kuathiri maisha ya wananchi wa Tanzania. Vile vile nirudie kutoa pole kwa watoto wetu ambao wamepoteza maisha wakati wakiwa kwenye harakati zao za masomo wakielekea huko kwa ajili ya kufanya mitihani ya kujipima wao wenyewe. Mwenyezi Mungu awalaze mahali pema peponi.
Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai, maji ni utu, maji huleta heshima na ustawi kwenye familia; lakini siyo familia pekee, bali na jamii kwa ujumla. Kwa mantiki hiyo, tunaamini kwamba Tanzania ina changamoto kwenye eneo hili la maji. Kila mtu kwa njia moja au nyingine anaguswa na changamoto hii ya maji, iwe ni wa mjini iwe ni wa kijijini anaguswa na changamoto hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa zaidi changamoto hii inamgusa mwanamke, kwa sababu mwanamke ndiye mtafutaji wa maji katika familia. Kama nyumbani hakuna maji, mwanamke hawezi kukaa kitako; lazima atoke sehemu moja hadi nyingine kuhakikisha kwamba amepata maji ili maisha yaendelee.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mantiki hiyo, tunaiomba Wizara ya Maji iongeze hiki kiwango, lakini kama siyo kuongeza, tuangalie vyanzo vingine ambavyo vitatusaidia kuongeza hii bajeti yetu ya maji. Kama Waheshimiwa Wabunge wengine waliotangulia walivyosema, tuchukue ile tozo ya sh.50/= tuongeze kwenye maji hatimaye tuwe na sh.100/=. Tukiweka sh.100/= itatusaidia kuongeza bajeti yetu. Kwa mantiki hiyo basi, ile bajeti ya mwaka 2016 ndiyo irejee na kuwa bajeti ya mwaka huu kwa taratibu zake zinazohusika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naelekea kwenye Jimbo letu la Lindi Mjini. Tatizo la maji kwenye Jimbo la Lindi Mjini ni kubwa, tena sana. Lindi Mjini hakuna maji, Lindi Mjini hali ni tete. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikuja Lindi na akasema ifikapo tarehe 3 Julai, lazima tuhakikishe kwamba maji yamepatikana. Serikali mtuambie, je, maji yatapatikana au hayatapatikana? Tunasubiri kauli ya Serikali ili mwanamke huyu tumtue mzigo.
Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Naomba mengine niyaandike kwa maandishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa hii fursa. Sambamba na hilo naomba nikupongeze kwa kukalia hicho Kiti ili kuweza kuliongoza Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzanaia, Mwenyezi Mungu akubariki sana, Allahu zidna I’lmi wa Ruzukna fahma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa, kwa hotuba yake nzuri ambayo ameitoa kwenye Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni hotuba nzuri ni hotuba ambayo imeeleza mambo mengi ambayo yanawagusa Watanzania wote. Hongereni sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya ni kazi iliyotukuka, kazi hii anaifanya ndani ya nchi yetu ya Taifa letu la Tanzania na nje ya mipaka yetu Afrika na Duniani kote kwa ujumla. Hongera sana Mama tunakuamini, tunakupenda sana tuko bega kwa bega na wewe kuhakikisha kwamba kila dhamira uliyokuwa nayo tunakuunga mkono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika Bunge hili au katika nchi yetu ya Tanzania hasa Wabunge ambao ndiyo wawakilishi wa wananchi, hakuna Mbunge yeyote humu ndani atakayesimama bila kueleza mazuri aliyoyafanya Mheshimiwa Rais katika Jimbo lake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye elimu amefanya makubwa, ukienda kwenye maji amefanya makubwa, ukienda kwenye maji amefanya makubwa, ukienda kwenye barabara amefanya makubwa, ukienda kwenye michezo ndiyo funga kazi amefanya makubwa sana. Kwa hiyo, tunakupongeza sana Mama yetu Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo nataka kuchangia kwa kuanzia na eneo lifuatalo: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, unyanyasaji wa watoto, ndoa za jinsia moja, malezi na makuzi ya watoto wetu. Kwa nini nimeanzia katika eneo hili? Nina sababu kubwa ya msingi. Bila watoto hakuna Taifa, watoto ndiyo Taifa letu na ndio tegemeo letu. Watoto ndiyo baraka ambayo Mwenyezi Mungu ametupatia wanadamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutasema Mama amefanya kila kitu katika Taifa letu, shule nani anatakiwa aende? Anatakiwa aende Mtoto! Hospitali watoto wanatakiwa waende, barabara watoto wanatakiwa wazitumie, kila kitu kinatutegemea sisi na kinawategemea watoto hawa. Leo sisi ni Wabunge ambao tuko humu ndani, tufikirie kwamba una mtoto wako umemuacha huko nyumbani unaambiwa mtoto huyu sasa hivi ameingia kwenye kulawitiwa, kama mzazi kama mlezi unajisikiaje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepewa dhamana ya kuwalinda, kuwatetea na kuwasemea. Kwenye hili ni jambo ambalo hatukubaliani nalo kama Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwenye jambo hili tusiletewe vitu kutoka huko, sisi kama Watanzania tunao utamaduni, mila na desturi zetu ambazo ndizo zinatuongoza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huu Wabunge hili ni jambo la kulaaniwa. Ni lazima kama Wabunge tuwe na azimio la kulikataa hili jambo sisi ndiyo waamuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaniuma sana na Watanzania inawauma sana. Nikiwa Mke wa Rais siyo sasa hivi nimeondoka kwenye kuwa Mke wa Rais isipokuwa sasa hivi ni Mstaafu, nilikuwa na Taasisi yangu na inaendelea Taasisi ya Wanawake na Maendeleo kauli mbiu ilikuwa ‘Mtoto wa Mwenzio ni Mwanao’. Maana yake ni kwamba Mtoto wa Mwenzio akiwa mwanao utamtendea vitendo viovu? Huwezi kumtendea, utamlinda na katika kumlinda kule utamtengenezea maisha ya baadae. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo dunia kuna baadhi ya watu wanatengeneza utaratibu wa kuzaa watoto wawili. Sisi tulikuwa tunazaa watoto wengi, dunia hiyo hiyo leo wanatuletea ndoa za jinsia moja, hivi tutakuwa na kizazi sisi? Mwanaume akishafanyiwa kitendo cha namna ile basi hawezi kufanya kazi, atapata wapi watoto? Hawezi kupata watoto. Kwa muktadha huo ni lazima jambo hili tulikemee vikali kadri inavyowezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo kwa sababu wenzangu wengi wamesema na mimi niishie hapo. Hili jambo hatulitaki sehemu yoyote nitakayosimamishwa duniani nitasema hili jambo silitaki na silitaki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu elimu, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati anatoa taarifa yake alizungumzia suala la shule 26. Miongoni mwa shule 26 shule 10 ziko tayari na ziko ndani ya Mikoa 10. Mikoa hiyo ni pamoja na Mkoa wa Dar es Salaam, Mkoa wa Lindi, Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Pwani na Mikoa mingine ambayo inafanya idadi kuwa shule 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachopenda kusema shule hizi ziko kumi na kila shule ni bilioni nne. shule hizi ni pesa za walipakodi wa nchi nchi hii ninachokiomba au ninachoshauri au kabla ya hapo mwezi wa saba mwaka huu zinaanza kuingiza wanafunzi wa kidato cha tano lakini katika uwasilishaji sikuona hata shule moja ambayo tungeona tu kwa mfano wakati wanatoa taarifa wanaonesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba, nilikuwa kwenye Kamati ya Kudumu na Maendelaeo ya Jamii, sasa hivi niko katika kamati nyingine. Tulikuwa na lengo la kwenda kuzitembelea shule hizi hatujaweza kuzitembelea. Siamini kama kuna kamati imekwenda kuzitembelea. Ushauri wangu kamati hatawakiwa watu wachache waende wakazitembelee shule hizi kabla ya mwezi wa saba kuona je zina ubora? Ubora upo, je inawezekana mwezi wa saba au laa! Ushauri wangu waende wakazitembelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hizi shule tunaambiwa zimeisha ni kweli, mimi kwenye jimbo langu shule hii ipo ndani ya Jimbo langu la Mchinga. Ninachoshauri waweke ukuta yaani uzio kwa ajili ya kuwalinda mabinti hawa kwa sababu tunataka wasome vizuri na mabinti hawa ni mabinti wenye vipaji maalum lakini kwenye eneo la sayansi tunawahitaji wanasayansi wengi zaidi katika Taifa letu la Tanzania kwe sababu hii ni Tanzania ya Viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nataka nizungumze kidogo kwenye suala la uvuvi, na uvuvi huu unawahusu sana vijana, wanaovua ni vijana, Ukanda wa Pwani una vijana wengi zaidi hata kwenye Jimbo langu la Mchinga kuna upande mzuri haujawahi kuokea nafikiri ni eneo la kwanza hata katika nchi yetu ya Tanzania, kuna beach nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba au ninachoshauri hao vijana uchumi wao mkubwa wanategemea Bahari, kule kuna Bahari hakuna mito, sasa vijana hawa wakopeshwe aidha maboti kwa ajili ya kujenga uchumi wao kwa ajili ya kipato chao, na si maboti tu na vitendea kazi vingine wakopeshwe watakuwa na uwezo wa kulipa kwa sababu watakwenda eneo la mbali kutafuta riziki lakini ukiwa na kile kimtumbwi hauendi mbali na unachokipata siyo kikubwa huo ndio ushauri wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka nizungumzie maliasili na utalii nilisimama hapa nikazungumzia suala la kuongezeka kwa tembo, na nilichangia hiyo hoja kuhusu tembo nikasema tembo ni wazuri sana tembo ni Wanyama ambao wanatuongeza fedha za kigeni tembo hao. Lakini watu wengi wanaopitiwa na tembo tembo siyo rafiki, tembo hii njaa ambayo sasa hivi inazungumzwa tumeletewa mahindi, ni kwa sababu maeneo mengine ni kwa sababu ya tembo wanakula vyakula. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunaishukuru Serikali kwa kutuletea mahindi kupunguza ile njaa. nitakuwa ni mchoyo wa fadhila nisipoweza kuipongeza Serikali, Serikali imenitendea mambo mengi makubwa na mazuri miongoni ni kwenye hilohilo la hao Wanyama tembo hao, niliwaomba gari, wameniletea gari jipya Jimbo la Mchinga, niliwaomba kile kituo ambacho maaskari watakaa kwa ajili ya kuwadhibiti tembo na kuwafukuza wamenijengea kituo kizuri ajabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo wakati huo kulikuwa na maaskari wawili nikasema maaskari wawili watawezaje kudhibiti tembo 30 sasa hivi wameniletea maaskari zaidi ya 20. Kwa hiyo, ninawashukuru sana. Lakini sambamba na hilo kwa wale ambao watanzania wale ambao wanapitiwa na yale maeneo ambayo tembo wapo wasaidieni watanzania wanashida tena shida yao siyo ndogo shida kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo niwashukuruni sana nimshukuru sana Mheshimiwa Rais nina mambo mengi nitakuja kuyasema nitakapo changia Wizara nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na wataalam wote wa Wizara kwa kazi nzuri ya kuwapatia Watanzania umeme takriban nchi nzima.
Mheshimiwa Spika, katika Jimbo letu la Mchinga, tuna maeneo kadhaa ambayo hayajafikiwa na umeme. Maeneo hayo ni Kijiji cha Ruvu (Kata ya Mchinga), Kijiji cha Dimba(Kata ya kilolambwani), Kijiji cha Matapwa(Kata ya Mipingo), Kijiji cha Mnyangara (Kata ya Mipingo), Kijiji cha Lihimilo (Kata ya Mipingo)na Kijiji cha Namkongo (Kataya Mipingo).
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.
MHE. SALMA J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama ili niweze kutoa mchango wangu kwa Taifa langu. Pili, nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa utendaji wake mahiri wenye nia thabiti ya kuwaletea Watanzania maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nawapongeza Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kusimamia sekta ya afya hapa nchini. Nina faraja kubwa kwamba juhudi wanazofanya katika kusimamia sekta ya afya zinaonesha matunda chanya. Nina imani kubwa na utendaji wao na sina shaka kwamba sekta ya afya chini yao itaendelea kuimarika siku hadi siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuongelea jitihada katika kupambana na vifo vya wanawake na watoto. Tafiti mbalimbali zilizofanywa na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali zimeonesha kuwa Tanzania imejitahidi kwa kiasi kikubwa katika kupambana na tatizo la vifo vya akinamama na watoto walio chini ya miaka mitano. Jitihada hizi ni matokeo ya hatua za dhati zilizochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha kuwa inaimarisha huduma mbalimbali katika sekta ya afya kama vile upatikanaji wa vifaa tiba, chanjo za watoto na huduma za kinga pamoja na tiba za magonjwa kama vile kuharisha, utapiamlo, surua, malaria na maambukizi katika mfumo wa upumuaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na jitihada zilizofanyika katika kupambana na vifo vya akinamama wajawazito na watoto walio na umri chini ya miaka mitano bado kumekuwa na changamoto mbalimbali. Changamoto hizi zimebabishwa na matatizo kama vile upatikanaji wa huduma bora za dharura za uzazi kwa akinamama hasa maeneo ya vijijini ambapo akinamama wajawazito wengi hufariki kwa kukosa huduma za upasuaji wa dharura wakati wa kujifungua; upatikanaji wa damu salama kwa akinamama ambao hupoteza damu nyingi wakati wa kujifungua; hali duni ya akinamama wajawazito hasa maeneo ya vijijini ambapo huhitajika kwenda na vifaa kama vile gloves, pamba, sabuni
na vifaa vingine vya kujifungulia jambo ambalo huwafanya akinamama wengi kuamua kujifungulia kwa wakunga wa jadi ambao baadhi yao hawakupata mafunzo ya kutoa huduma za uzazi; utoaji wa mimba usio salama na kifafa cha mimba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza jitihada katika kukabiliana na vifo vya akinamama na watoto vinavyotokana na changamoto zinazojitokeza katika sekta hii ya afya ya mama na mtoto, ni vyema Serikali ikachukua hatua zifuatazo:-
(i) Kuhamasisha jamii itoe taarifa kuhusu ubora wa huduma za afya kwa mamlaka ya Serikali za Mitaa ikiwa ni pamoja na kueleza hali ya upatikanaji wa wataalam wa afya na hali ya matibabu;
(ii) Kusaidia katika kujenga uwezo wa mfumo wa afya wa wilaya ili kuwezesha katika utoaji na usimamiaji wa huduma bora za afya ya uzazi, ikiwa ni pamoja na uzuiaji wa maambukizo ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto;
(iii) Wizara ihakikishe kunakuwa na dawa za kutosha kwa ajili ya kuzuia maambukizi ya VVU kwa akinamama wajawazito ili kusaidia katika kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa watoto kwa lengo la kuwezesha watoto wengi zaidi kuzaliwa wakiwa salama;
(iv) Kuhamasisha jamii na familia kuunga mkono wanawake na kuwawezesha kuwa na kauli katika masuala yanayohusu huduma zao za afya; na
(v) Serikali kwa kushirikiana na vyombo vya habari itetee kwa nguvu ongezeko la uwekezaji katika huduma za afya ya wanawake katika ngazi ya Taifa na ya Serikali za Mitaa kwa kutumia vielelezo vinavyoonesha maafa na athari ya vifo vya wanawake vinavyotokana na uzazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kampeni ya kuzuia maambukizi ya virusi vya UKIMWI toka kwa akinamama kwenda kwa watoto. Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara imekuwa katika vita dhidi ya maambukizi mapya ya Virusi vya UKIMWI hasa upande wa maambukizi ya UKIMWI toka kwa mama kwenda kwa mtoto. Takwimu zinaonesha kuwa idadi ya watoto walio chini ya umri wa miaka mitano ambao wanakufa kutokana na maambukizi ya virusi vya UKIMWI kutoka kwa mama zao ni kubwa. Serikali inapaswa kufanya jitihada kubwa za kuhakikisha inaokoa maisha ya watoto hawa ambao ndiyo nguvu kazi ya Taifa la kesho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha jitihada hizi zinafanikiwa, ni vyema Serikali ikahakikisha kuwa:-
(i) Inatoa programu nyingi za uzuiaji wa maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (na kinga nyingine) zikiwemo programu za kuwasaidia wanawake kuwa na afya kwa muda mrefu kwa msaada wa lishe na matibabu;
(ii) Kutoa mafunzo kwa wanasihi wengi, wafanyakazi wa jamii wa kujitolea na wakunga wa jadi ili kuwafikia wanawake wengi na taarifa za kuaminika na ushauri kuhusu mambo ya kufanya wanapokuwa na maambukizi ya VVU. Wanawake wanaoishi na VVU wanahitaji kujua nini cha kufanya, kwa mfano, kuepuka mimba zisizotakiwa na hatari zinazoweza kutokea kwa watoto wachanga kutokana na lishe duni na maambukizi yanayohusiana na ulishaji mbadala; na
(iii) Kuboresha hali ya huduma za afya ili kuhakikisha kuwa watoto wachanga hawaambukizwi wakati wa kuzaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Pia nitoe pongezi kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya katika kuboresha elimu. Pamoja na hayo, niwapongeze Walimu wenzangu wote nchini Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya katika sekta hii ya elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, niwapongeze Walimu wenzangu, wengi wao wameweza kujiendeleza katika maeneo tofauti kuanzia ngazi za chini, hadi kufikia eneo lingine la Masters na Ph.D, hongereni sana Walimu wenzangu popote pale mlipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia suala la elimu na tunazungumzia uboreshaji wa elimu. Tunasema kwamba tunataka tuboreshe; katika maboresho haya, ninachokizungumzia, Walimu hawa wanapojiendeleza ni vema kabisa baada ya kumaliza masomo yao, wasiombe nafasi za kwenda aidha Sekondari au kwenye Vyuo. Kwa sababu tuko kwenye maboresho, msingi wowote ni muhimu sana katika jambo lolote lile. Kwa hiyo, Walimu hawa ni vema wabaki kwenye zile shule kama ni wa Msingi wamejiendeleza wamepata Diploma au wamepata Degree wabaki pale, lakini kitu kikubwa ni vema kabisa Walimu hawa waboreshewe maslahi yao kulingana na elimu yao waliyokuwanayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuje kwenye eneo la Mafunzo ya Ualimu. Nimeona Walimu wengi wamepata fursa juu ya maeneo hayo, lakini sijaona mafunzo kwa eneo la Elimu ya Awali. Sera inatuambia kwamba kwenye kila Shule ya Msingi kuwe na darasa la elimu ya awali. Sasa kama tunataka tuboreshe, ni lazima tuanzie kuboresha kwenye Elimu ya Awali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ithibati katika ukurasa wa 19 aya ya 37. Tumeambiwa kwamba kulikuwa na suala zima la ukaguzi, Walimu 7,727 walikaguliwa; Msingi 6,413, Sekondari 1,314. Ni vema kabisa, lakini lengo ilikuwa kukaguliwa Walimu 10,818. Hawa ni baadhi tu ya waliokaguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukija kwenye eneo hili, ili tuweze kuboresha elimu yetu hapa nchini Tanzania, hili eneo la ukaguzi ni lazima lipewe kipaumbele. Kuwe na pesa ya kutosha na kuwe na vitendea kazi. Ili kuboresha eneo hili, ni lazima Walimu wakaguliwe mara kwa mara. Unaweza ukakuta ndani ya miaka; nazungumza haya kwa sababu nina uzoefu juu ya eneo hili, mimi ni Mwalimu kwa taaluma. Unaweza ukakuta zaidi ya miaka miwili au mitatu Mwalimu hajakaguliwa. Sasa unategemea ubora wa elimu hapa utakujaje kama hakuna mtu wa kumsimamia huyu Mwalimu? Kwa hiyo, hili eneo ni lazima lipewe kipaumbele cha namna ya pekee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyazungumza haya, napenda nizungumzie eneo la Shule ya Lindi Sekondari. Nimeona maeneo mengi wameboreshewa, wameambiwa itaboreshwa hili, itatengenezwa Shule hii, itafanya hivi, lakini Sekondari ya Lindi ilipata tatizo la kuungua moto; na moto ulikuwa mkubwa na ulipoteza karibu madarasa yasiyopungua sita pamoja na eneo la Mikutano. Serikali hapa mnatuambiaje juu ya shule hii iliyoko Mkoa wa Lindi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la mimba. Suala la mimba ni tatizo na suala la utoro ni tatizo. Sisi kama wanawake tunawapenda sana na ni lengo letu Waheshimiwa Wabunge wanawake kuwatetea watoto wa kike na mwanamke yeyote yule ambaye anaomba nafasi ya uongozi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili la mimba, hasa mimba za utotoni, sikubaliani na kwamba watoto wakipata mimba warudi tena shuleni. Hili sikubaliani nalo hata kidogo! Sababu za kutokukubaliana nazo ni hizi zifuatazo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunazungumzia suala la mila, desturi, utamaduni na mazingira…(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na dini. Hakuna dini yoyote inayomruhusu mtoto wa kike kupata mimba kabla ya wakati. Biblia inasema na Quran inasema. Tunapofanya mambo yetu ya msingi tuangalie vilevile mambo yanayohusu imani zetu za dini. Suala la mtoto kurudi shuleni, tutafute njia nyingine mbadala. Sisi kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuna Kanuni zetu na ndizo tunazozifuata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika kwenye suala la mimba, sheria inayofuata hapa mtoto akipata mimba asirudi shuleni. Kama hapa ingekuwa sisi kama Wabunge hatuna sheria na kanuni, ingekuwa tunafanya mambo kila mtu na jambo lake, lakini sheria zinatubana. Nataka kwa hilo sheria zibane. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka sheria ibane. Mtoto akipata ujazito asirudi shuleni, atafutiwe njia nyingine ya kuweza kumsaidia mtoto huyu.
TAARIFA...
MHE. SALMA R. KIKWETE: Nashukuru sana kwa kuniunga mkono. Naomba wanawake wote waniunge mkono na wanaume vilevile waniunge mkono. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi? Kama hivyo ambavyo sisi tunawatetea...
MHE. SALMA R. KIKWETE: Tuwatetee katika mazingira…
TAARIFA...
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Taarifa hiyo siikubali, naikataa…
(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)
MHE. SALMA R. KIKWETE: …pamoja na kwamba kwamba watoto hawa wanapata mimba katika umri mdogo; lakini ni lazima tuwatengenezee mazingira wezeshi. Mazingira wezeshi tukisema warudi shuleni watoto hawa, ina maana wengi watapata mimba.
(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Wengi watapata mimba katika umri mdogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Sambamba na hilo, nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya. Kazi hizi nzuri zinazofanywa tukiziainisha hapa ni nyingi na kwa wingi wake huo kumekuwa na mafanikio makubwa sana ndani ya kipindi chake cha uongozi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, niwapongeze Mawaziri wetu wa Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Kwa ujumla bajeti hii ya Serikali imegusa kila sehemu yaani bajeti ya wananchi. Wananchi wamepunguziwa kwa kiasi kikubwa sana na bajeti inayoonyesha muelekeo na mwelekeo huu ni ushindi wa mwaka 2020 na hatimaye kuelekea kule mbele ya safari 2025, ongezeni hizo juhudi ili tufike 2025, na hatimaye tuzidi kusonga mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye maeneo kama mawili/matatu hivi. Eneo la kwanza, wakati Waziri anasoma bajeti ya Wizara ya Fedha alielezea suala la kinu cha kuchakata gesi pale Lindi ambacho kinu hiki kiko eneo linaitwa Likong’o. Baada ya hapo kwa kweli nilipiga sana makofi na nilipiga hili benchi nafikiri watu wengi walisikia. Msingi wangu mkubwa ni kwamba kinu kile kikipelekwa pale matokeo yake tunazungumzia hii nchi ni nchi ya viwanda, na ikiwa ni nchi ya viwanda na wananchi wa Lindi wale watafaidika na kauli mbiu hii ya Awamu ya Tano kwamba iwe ni nchi ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini limetokea? Wakati anaisoma hii bajeti ya Serikali ambayo ndio inayotoa mwelekeo nini kinafanyika ndani ya Taifa, hakukuwa na jambo lolote lililojitokeza juu ya kinu kile na wananchi wa Lindi wanasubiri. Hata kama sio leo au kesho, lakini wapewe mwelekeo ni nini kinafanyika. Kikubwa zaidi hii ni gesi na gesi itaongeza uchumi wa Lindi, kiwanda kile kikijengwa Lindi kama Lindi hakuna kiwanda hata kimoja. Wananchi wa Lindi ni maskini lakini sio maskini kwa sababu hakuna rasilimali, ni kwa sababu mimi naamini wakati ulikuwa haujafika na sasa wakati umefika na wananchi wale wa Lindi kufurahia matunda ya nchi yao. Naomba atakapokuja Mheshimiwa Waziri anipe mwelekeo nini hatima ya kinu kile cha kuchakata gesi ndani ya Mkoa wetu wa Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maji. Nilizungumzia suala la maji, sasa ninachosubiri hapa ni matokeo. Je, kati ya tarehe 3 mpaka 10 mwezi wa saba maji haya yatapatikana au hayatapatikana, kwa sababu maji ni kilio kikubwa sana ndani ya Mkoa wa Lindi hasa Wilaya ya Lindi Mjini na maeneo yake ya jirani. Tanzania tumejaliwa tuna mito, mabonde na tuna maziwa, kama tukiwekeza vizuri matatizo haya yatapungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niende kwenye eneo la elimu. Mimi kwa taaluma ni mwalimu, sasa hii naiomba niishauri Serikali. Unajua sisi tuna senti, inaanzia senti tano hatukuanzia na senti moja mpaka senti mia moja. Ninachoishauri mimi kama mwalimu nilikuwa napata changamoto na hii changamoto inazidi kuendelea. Wakati zinatengenezwa zile fedha zitengenezwe hizi senti tano, ukiingia leo darasani kumfundisha mwanafunzi senti tano, senti 20 na senti 50 zinafananaje. Ni lazima tumuonyeshe kitu kwa uhalisia, tupeleke vitu wanafunzi wajifunze, hili ni muhimu sana ili wanafunzi waweze kutambua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la elimu kwa kweli tumepiga hatua, tumefanya mambo mengi sana kwenye elimu kwa kipindi kifupi. Tumeboresha shule zote zina madawati, upande wa walimu wa sanaa wote wamejaa, lakini tatizo sasa ni baadhi ya walimu kwenye maeneo ya sayansi. Sasa hapa ni lazima tuwekeze vya kutosha ili watoto wetu wafanye kazi kwa vitendo, halafu hii nitairudia tena na walimu wale ambao wamejifunza na hatimaye wakapata aidha Shahada au Diploma zao wasiendelee kwenda kwenye vyuo kwa sababu lengo ni kuboresha elimu, wabaki kwenye shule zile za msingi, jambo kubwa hapa waboreshewe mahitaji yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tatizo lingine kubwa, kuna suala zima la nyumba za walimu bado hapa tupo nyuma. Kwa kuwa tuna tatizo la nyumba za walimu, vijana wengi hapa wamezaliwa katika mazingira ambayo sisi tunayajua, sasa kijana aliyezaliwa na kukulia Dar es Salaam leo hii umpeleke kule Chikonje ambako mimi ndio nilianzia ile kazi yangu kwa mara ya kwanza, akifika akiangalia, akisikia yale mabundi na wanyama wengine wanalia mwalimu anakusanya na anaondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, lakini nitakuwa ni mtovu wa fadhila… (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Hatimaye nikushukuru wewe Mheshimiwa Naibu Spika kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye Wizara hii ya Afya ambayo ni muhimu sana kwa ustawi na maendeleo ya mwanadamu katika muktadha ufuatao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, usipokuwa na afya njema huwezi kwenda shule; usipokuwa na afya njema maendeleo hayawezi kufanyika; usipokuwa na afya njema kitu kitakachojitokeza hata uchumi wa Taifa letu utapungua kwa ajili ya kukosa nguvu kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya katika Taifa letu. Sambamba na hilo namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Afya pamoja na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara hii bila kuwasahau madereva na wahudumu ambao wanafanya kazi nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii kwa kutupatia fedha kiasi cha shilingi 1,200,000,000 katika Jimbo la Lindi Mjini. Shilingi milioni 400 zimetolewa kwa ajili ya Hospitali ya Kituo cha Afya cha Mingoyo, lakini shilingi milioni 700 zimetolewa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Mnazi Mmoja. Tunaishukuru sana Serikali.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, pamoja na mazuri ambayo yameweza kujitokeza, lakini Lindi tuna mambo yafuatayo; hatujajua hatma yetu ya Mkoa wa Lindi kuwa na Hospitali ya Mkoa na Hospitali ya Wilaya. Ukiuliza hivi, unaambiwa Sokoine ni Hospitali ya Mkoa. Wakati mwingine unaambiwa Sokoine ni Hospitali ya Wilaya. Mheshimiwa Waziri, naomba utakapokuja hapa utupe ufafanuzi juu ya jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kama Mkoa wa Lindi na kama ambavyo Hospitali ya Sokoine iko pale, lakini kikubwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa hana gari la kufanyia huduma. Sizungumzii ambulance, tunazungumzia gari la kufanyia huduma, anatumia gari binafsi kuendeshea shughuli za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 28 tu ndiyo ya wahudumu waliopo ndani ya Mkoa wa Lindi. Tuna upungufu wa asilimia 72. Naomba hili liangaliwe kwa jicho la huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya UKIMWI nchini Tanzania kwa mujibu wa Tanzania HIV Impact Survey ya mwaka 2016/2017, maambukizi ya wanawake ni asilimia 6.5 na wanaume ni asilimia 3.5. Hii hufanya maambukizi Kitaifa ni 5%. Sasa ndani ya Mkoa wa Lindi ni asilimia 0.3. Nawapongeza sana watu wa Mkoa wa Lindi kwa kupunguza kiasi kikubwa cha maambukizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maambukizi ya UKIMWI yana vitu mbalimbali ambavyo vinasababisha. Kwa hiyo, tuna wajibu sisi kama Watanzania kuepuka vitu vile ambavyo vinaambukiza ili pesa hizi zitakazopatikana baada ya kutumika kununua madawa na vitu vingine, zitumike katika mazingira ya kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia ARVs ndiyo dawa zinazotumika kufubaisha virusi vya UKIMWI. Sasa hizi dawa ziende kwa wakati kwa kunusuru maisha ya watu hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu vifo vya akina mama na watoto; haikubaliki nchi kama Tanzania, mwanamke kufa wakati analeta kiumbe kingine duniani. Tunajua kuna mipango na mikakati mizuri sana iliyowekwa, lakini ni lazima itekelezwe na iwekwe kwa wakati. Kuna magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama figo, pressure na kisukari. Ni lazima yawekewe mikakati madhubuti ili kuhakikisha mazingira haya yanakuwa salama katika nchi yetu. Yote haya yanawezekana tu kama bajeti iliyopangwa na Serikali itapelekwa kwenye maeneo husika kwa wakati na ikiwa timilifu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja.
Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza kabisa, naomba niunge mkono Azimio la Bunge Kuridhia Ubadilishaji wa Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika-Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa. Naunga mkono Azimio hili kwa sababu zifuatazo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, katika mapori haya kwa kweli hali ya kiusalama kwa wananchi wakati wanasafiri kutoka eneo moja hadi lingine ilikuwa si yenye mazingira rafiki. Watu wakisafiri ilikuwa ni lazima kuwe na wasindikizaji kwenye maeneo hayo. Kwa kuipandisha hadhi ina maana hali ya usalama itakuwa imeboreka zaidi na ni jambo zuri kwa maeneo yale na ni jambo zuri kwa wananchi wetu wa Taifa letu la Tanzania kwani kila mtu anahitaji usalama, anahitaji kuishi na anahitaji ulinzi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hali kadhalika kwenye mapori haya ambayo yamepandishwa hadhi majirani zetu au watu wa maeneo mbalimbali waliweza kuyavamia na kuyamiliki kuwa ya kwao. Kwa muktadha huu sasa hivi hawataweza kuyavamia tena kwa sababu yako chini ya TANAPA watayaangalia katika mazingira bora zaidi. Sambamba na hilo, maeneo haya ni muhimu sana katika uchumi wa Taifa letu na maeneo yale yanayozunguka. Maeneo haya ni mazuri kiutalii kwa sababu ndani yake kuna maziwa, Uwanda wa Savana na vyanzo vya maji ambavyo ni muhimu sana katika mazingira ya kiutalii na wananchi ambao wapo katika maeneo yale. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tukizungumzia Geita kama Geita kuna Uwanja wa Ndege mkubwa ambao unajengwa. Uwanja huu kwa maeneo haya kupandishwa hadhi hautakuwa tena uwanja ule ambao unaitwa white sleeping giant au shite sleeping elephant matokeo yake watalii kutoka maeneo mbalimbali watautumia uwanja ule na utaweza kuleta tija kwa Taifa letu. Kwa hiyo, ni muhimu sana kwa maeneo haya kupandishwa hadhi ili kuweza kuleta mazingira bora na rafiki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, siku za nyuma kuliwekwa maazimio ya maeneo ya Kusini kuwa ni maeneo ya kiutalii, wakati tunazungumzia maeneo haya tusiyaache yale maeneo ya Kusini kwa sababu Kusini kama Kusini iliachwa nyuma kwa muda mrefu. Kwa hiyo, nachoshauri ni lazima yale maeneo ya Kusini yapewe kipaumbele, wakati huku tunatoa kipaumbele na kule kutolewe kipaumbele kwani Tanzania ni moja na sote ni wamoja.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kurudia tena kuunga mkono hoja. Ahsanteni sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, nikushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia Wizara hii muhimu kwa ustawi na maendeleo ya wananchi wa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba nitoe pongezi zangu za dhati kwa Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya ya kutatua tatizo la maji hapa nchini. Natambua na sote tunatambua kwamba wakati tumepata uhuru na baadae, nchi yetu ilikuwa na watu wachache, sasa hivi watu ni wengi sana na kila mwananchi ana mahitaji makubwa ya maji. Kwa jinsi hiyo, bado maji ni tatizo kwa wananchi wengi wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo Serikali imefanya juhudi kubwa na ya dhati kabisa kuweza kutatua matatizo ya maji katika maeneo kadhaa ya Taifa letu. Hakuna mtu ambaye anaweza kutatua tatizo hili kwa wakati mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, alianza Baba wa Taifa akafanya kazi yake, akaja Mzee Mwinyi akafanya kazi yake, akaja Mzee Mkapa akafanya kazi hiyo, akaja Mheshimiwa Mstaafu, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, mume wangu akafanya kazi yake na sasa hivi yuko Dkt. John Pombe Magufuli anafanya kazi yake na ataiacha hii na bado kazi itaendelea. Tunaamini Serikali ina dhamira ya dhati kabisa kuondoa tatizo la maji hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo sasa naomba nielekee kwenye eneo langu ambalo nalifanyia kazi kule Lindi. Naipongeza na kuishukuru sana Serikali kwa mradi mkubwa kwa mabilioni ya pesa ambao walitupatia na hatimaye leo hii wananchi wa Wilaya ya Lindi Mjini wanapata maji. Tatizo kubwa lililopo hapa pamoja na kupata yale maji, kuna tatizo dogo siyo kubwa sana, naamini wataalam wakikaa, aidha, Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Nishati wanaweza kutatua tatizo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo kubwa la kukatikakatika kwa umeme ndiyo linasababisha pump zisiweze kupeleka maji kwenye matenki hatimaye maji yale yakapelekwa kwenye maeneo husika. Naomba Wizara hizi mbili zikae kwa pamoja ili waweze kutatua tatizo hili ambalo linawakabili wananchi wa Wilaya ya Lindi Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishukuru Serikali kwa dhati kabisa kwa kutupa fedha kiasi cha shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya miradi mikubwa miwili; ujenzi wa miundombinu ya maji safi katika eneo la Ng’apa na Mitwero. Fedha hizi au miradi hii itasaidia kuondoa changamoto ya maji kwenye maeneo hayo niliyoyataja. Unaweza ukaangalia ukurasa wa 188 jinsi ambavyo Serikali imeweza kutuona. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka niende kwenye eneo la umwagiliaji. Tunajua na tunatambua kwamba kupanga ni kuchagua, na eneo hili ni muhimu sana kwa usalama wa chakula hapa nchini. Mwananchi yoyote pamoja na kuhitaji maji anahitaji kula. Tukiangalia eneo la umwagiliaji ni eneo ambalo lina uhakika wa kutupatia chakula hapa nchini. Kwa mfano takwimu zinaonesha kwamba hekta 475,520 sawa na asilimia 24. Asilimia 24 hii inachangia chakula kinachopatikana hapa nchini. Sasa kama tukiongeza mara mbili yake ina maana kwamba tutakuwa na asilimia 48 na asilimia hizi 48 zitatuongezea kiasi kikubwa cha upatikanaji wa chakula hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Upotevu wa Maji. Tunaamini na tunajua kwamba maji mengi yanapotea. Sasa katika hili ni lazima Serikali ichukue hatua makini zaidi kuweza kuthibiti hayo maji. Lakini hasa kule majumbani, maji mengi yanapotea; tuwe makini kuwaambia vijana wetu maji haya yasipotee. Wakati mwingine kikombe moja kinatumia maji zaidi ya lita tatu au lita nne kusafishia. Hii haikubaliki na hili haliwezekani ni lazima tuwe makini katika udhibiti wa maji yetu haya.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naona muda umenitupa mkono, lakini naomba kuunga hoja hii kwa asilimia 100, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Mikopo; ni jambo lenye tija kuunganisha taarifa za Bodi ya Mikopo na TASAF, ili kuondoa utata au usumbufu kwa walengwa wakati wa uombaji wa mikopo hiyo. Kwa kuwa watu wanaohudumiwa na TASAF wanakuwa na namba, ni muhimu wapewe namba na barua ya kuwatambulisha wakati wa kuomba mikopo ili kuondoa utata huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la kutoa ushauri huu ni kuwa kuna wengine hufiwa na wazazi wao na kisha hupata kibali cha kifo. Kwa hiyo basi, ni vyema kibali cha kifo kitambulike wakati taratibu nyingine za kufuatilia cheti zinafanyiwa kazi kwani elimu ni haki ya kila mtoto wa kitanzania.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu hatimaye nikushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia Wizara hii muhimu sana ya kilimo. Tukiamini kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu la Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ifikapo mwaka 2025 tunategemea kwamba nchi yetu ya Tanzania itakuwa ni nchi ya kipato cha kati ikiongozwa na kaulimbiu yetu ya Tanzania ya viwanda. Hili ni jambo jema sana kwa ustawi wa Taifa letu la Tanzania. Pamoja na hayo ili tuweze kufikia azma yetu ya 2025 kuwa Tanzania ya viwanda ni lazima kama nchi tuwekeze sana kwenye kilimo na hasa kilimo cha umwagiliaji ambacho kinatupa uhakika wa kile ambacho tunatarajia kukifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingi duniani zilianzia kwenye kilimo hatimaye kukaja na mapinduzi ya viwanda, kwa mantiki hiyo tukiwekeza kwenye kilimo tutakuwa na uhakika wa kupata malighafi zitakazotusaidia kwenye viwanda vyetu hatimaye tutaweza kukua kwa kadri tulivyokuwa tunatarajia. Ushauri wangu kwenye jambo hili ni lazima tupange mikakati yetu vizuri ili azma yetu hii tunayoitarajia iweze kutekelezeka kama tulivyojipanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia kwenye eneo la ufuta. Ufuta ni zao kubwa na ni zao muhimu. Sisi kama Tanzania tunalima ufuta lakini kama Afrika vilevile nchi yetu ni nchi ya pili ikiongozwa na Ethiopia, pia hatuko nyuma kwenye dunia. Katika nafasi ya dunia sisi Tanzania tuko kwenye kumi bora. Kwa mantiki hiyo ina maana kwamba tukiwekeza vizuri kwenye ufuta, nini kitakachoweza kujitokeza, tunaweza kuzalisha wenyewe mafuta ambayo sasa hivi ni changamoto kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia ufuta wakulima wetu tuliwahamasisha sana juu ya kilimo cha ufuta na mazao mengine mbalimbali. Tatizo linakuja baada ya wakulima kuweza kulima vizuri lakini hata hiyo pesa yenyewe waliyotumia kulima wamekopa kwenye mabenki, inafikia hatua uuzaji inakuwa ni changamoto kubwa kwao. Kwenye eneo hili vilevile ninafarijika. Nimesikia kwenye taarifa hapa
kwamba, kuanzia sasa kuelekea siku zijazo ufuta nao utakuwa ni kati ya mazao ambayo yatauzwa kwa stakabidhi ghalani, ninaipongeza sana Serikali kwa kuweka ufuta kwenye stakabadhi ghalani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee kuhusu korosho. Korosho tunaamini na zao kubwa na ni zao ambalo linachangia uchumi wa Taifa letu la Tanzania. Lakini sasa korosho hii imeingiliwa na mdudu na mdudu huyu ni unyaufu wa korosho. Katika taarifa sikusikia eneo lolote, ni mkakati gani wameupanga juu ya kuondoa tatizo hili la unyaufu wa korosho. Korosho hizi zinalimwa Lindi, Mtwara, Tanga, Pwani na Mikoa mingi ambayo iko kwenye Ukanda wa Pwani na sasa hivi korosho litakuwa ni zao la Kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Lindi hakuna kiwanda hata kimoja, ina maana kwamba suala la korosho lisipowekewe mkakati wa kudumu wananchi wa Lindi watazidi kuwa maskini kwa sababu hawatakuwa na kipato chochote kile, kwa kuwa hakuna kiwanda hata kimoja.
Mheshimimwa Mwenyekiti, naomba nielekee kwenye zao la mbaazi. Mbaazi tuliwahamisha wakulima walime, wengi sana walilima kweli kweli. Lakini ikafikia wakati mbaazi zikakosa soko, Mkoa wa Lindi ni asilimia 20 tu kati ya mbaazi zote ambazo zimeweza kuuzwa nyingi zimeharibika na wananchi hawa ni maskini. Serikali tunaomba iwasaidie chochote ili waweze kuendelea na kilimo waweze kujipatia maslahi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo nakushukuru sana kwa kunipa fursa, lakini jambo lolote ni mchakato, naamini matatizo haya tukijipanga yataisha. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama ili niweze kuchangia kwenye Wizara hizi ambazo ziko mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nichukue nafasi hii kukishukuru chama changu, Chama cha Mapinduzi, kikiongozwa na jemedari wake Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo inafanyika katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, naomba nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Waziri wetu wa TAMISEMI kwa kazi kubwa na nzuri ambazo anazifanya, lakini sambamba na hilo kwa uwasilishaji wake ambao ni mahiri sana, pamoja na kwamba muda kwake ulikuwa ni mfupi, lakini nimpongeze kwa uwasilishaji wake na kazi nzuri ambazo anazifanya kila kona ya nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais mara alipochaguliwa au kabla ya kuchaguliwa aliwaahidi Watanzania kufanya kazi kwa umahiri na weledi mkubwa sana. Hii inaonesha kwamba Mheshimiwa Rais anawatumikia Watanzania. Ukiangalia kwenye kipindi ambacho kinasema tunatekeleza na kishindo cha Awamu ya Tano unaona jinsi kazi ambavyo zinafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ukiangalia tunatekeleza, unaona kila kona ya mkoa wa nchi yetu, kila wilaya, kila eneo na Mawaziri wote kwa pamoja wameshikamana kufanya hizo kazi ambazo zinaonekana katika nchi yetu; ama kweli Tanzania ya viwanda inaonekana na tunaamini itakapofika mwaka 2025 kwa kweli uchumi wa kati utafikiwa kabla ya huo mwaka ambao tunausema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa machache tu naomba niyaseme yafuatayo ambayo Mheshimiwa Rais na Serikali yetu imetekeleza; ujenzi wa Stiegler’s ambao utatusaidia kupata umeme wa bei nafuu na sisi tunaelekea kwenye nchi ya viwanda, ni lazima tuwe na umeme wa bei nafuu. Sambamba na hilo, kuna standard gauge, itarahisisha usafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine, vilevile, itapunguza matatizo ya barabara kwa sababu mizigo mingi inaposafirishwa kupitia barabarani maana yake ni kwamba barabara inaharibika na kila baada ya muda mfupi inabidi tutengeneze.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo, sisi tunahitaji watalii. Amenunua ndege ambazo sio kwamba watatumia watalii pekee bali hata sisi wenyewe ndani ya nchi tutazitumia. Na tunashuhudia, Jumatatu asubuhi watu wengi, kila mtu anahitaji ile ndege na watu wengine wanakosa, na hizo ndege watu wote tunazipanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ameanzisha Mahakama ya Mafisadi. Hili nataka nilisemee; Mahakama ya Mafisadi ilikuwa na umuhimu kwa sababu ni agenda ambayo ilikuwa imezungumzwa kwa kasi sana lakini Rais wetu na chama chetu ni sikivu, chama chetu kimetengeneza ilani ya kuvishughulikia hivi vitu na kweli Rais wetu kwa sababu ni msikivu vyote amevifanya, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna suala la elimu bure, elimu hii imeleta chachu ya watoto wengi wa Kitanzania kuingia shuleni. Kila kwenye mafanikio hakukosi upungufu na upungufu ndiyo chachu ya maendeleo. Kwa hiyo sasa tunachotakiwa ni kujipanga juu ya watoto wengi waliopo madarasani kwetu ambao wanakosa huduma muhimu za msingi. Na zote hizi zimeelezwa na jinsi ya kutekelezwa vilevile zimeelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuhusiana na elimu bure naomba nijikite kwenye suala hilohilo, tunaanzia elimu ya awali. Kwenye elimu ya awali ilani inasema kila kwenye shule ya msingi kuwe na darasa la awali na hii imetekelezeka kwa kiasi kikubwa. Jambo ambalo nataka nishauri, kwenye elimu ya awali ni lazima kuwe na Walimu ambao wana weledi wa kuwafundisha wale watoto wa darasa la awali kwa sababu kabla ya hapo tulikuwa hatuna hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake watoto walikuwa wanakwenda kwenye zile private schools wakitoka pale wakiingia darasa la kwanza matokeo yake wale wanaonekana kwamba wana maarifa zaidi kuliko hao kwa sababu hawakupitia elimu ya awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utafiti wanasema hakuna mtu ambaye uwezo wa akili ni mdogo isipokuwa wanatofautiana katika kuelewa, mwingine anaelewa kwa kiwango cha chini, mwingine cha kati na mwingine kwa kiwango cha juu. Kwa hiyo hii elimu ya awali imesaidia sana, hapa ni lazima wawepo walimu wenye weledi sio Walimu wapo basi anachukuliwa huyu nenda kafundishe elimu ya awali, hii sio sawa na haileti afya kwa suala zima la elimu na tukiamini kwamba elimu ndiyo msingi wa kila jambo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nizungumzie suala la elimu ya msingi; kwenye elimu ya msingi hapa ni lazima tuwaandae watoto wetu tangu mwanzo kuona kwamba hawa watoto wetu je, wanafaa kuwa akina nani, tuwaandae watoto kuwa Walimu kwa sababu kila kitu kinatengenezwa. Sasa kitu ambacho tunakiona unakuta kwamba, kwa sababu watoto hawaandaliwi kuwa Walimu ukienda ukauliza nani anataka kuwa malimu kila mtu ameshusha mkono chini, hataki kuwa Mwalimu kulingana na kutowaandaa na kulingana na mazingira yaliyopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hilohilo la Walimu, wamesema kuna Walimu wengi, ajira zimetoka; je, kati ya hizi ajira zilizotoka ni Walimu wangapi? Pamoja na kwamba wanasema wengine wamepelekwa kwenye eneo la wenye ulemavu, je, kwenye ulemavu mmeangalia watoto wenye usonji? Kwa sababu watoto wenye usonji ni wenye mazingira magumu, mtoto mwenye usonji unaanza kumtambua akiwa na umri wa miaka mitatu na ni watoto ambao kukaa nao ni mtihani, naomba tufanye utaratibu tuwaandae.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali haina shule hata moja yenye watoto wenye usonji. Al Muntazir wameanzisha hili darasa la watoto wenye usonji, hakuna ubaya Serikali ikashirikiana na Al Muntazir kuwasaidia watoto wenye usonji kwa sababu kila mtoto anayo haki ya kupata elimu kwa wakati muafaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la Walimu wa sayansi. Tatizo hili ni kubwa sana hapa nchini. Ni lazima tutengeneze mkakati wa kuwaandaa Walimu wa sayansi tangu ngazi za awali, hasa kwenye shule za msingi, tuwaandae watoto tujue huyu atakuwa Mwalimu wa sayansi. Kwa hiyo tuanze maandalizi haya mapema, hatimaye tutaondoa tatizo la Walimu wa sayansi. Pamoja na kwamba wameajiriwa Walimu zaidi ya 1,900, kati ya Walimu hawa je, Walimu wangapi ni Walimu wa sayansi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kama alivyosema pale mwanzo, maandalizi ya Walimu yaanze mapema baada tuwe na mkakati kwamba ndani ya miaka ama mitano au kumi tuwe na kazi ya kuwaandaa Walimu hawa ili tuwe na Walimu bora kuanzia elimu ya awali, elimu ya msingi mpaka elimu ya sekondari, hapa tutakuwa na matokeo mazuri na kama tunataka hayo maboresho. Tunaamini Serikali yetu ni sikivu haya yanawezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna suala zima la ukaguzi; nimepitia sikuona kabisa eneo la ukaguzi, au labda pengine nime-overlook, sikuona. Suala la ukaguzi ni muhimu, ni lazima kuwepo na Wakaguzi ili waweze kufuatilia kazi za Walimu, hatimaye ndiyo tutaona mafanikio ya elimu yetu. Hili kwa kuwa halipo ni lazima liwekwe kwa ajili ya ubora wa elimu ya watoto wa nchi yetu, bila ukaguzi hakuna kitu, nazungumza hayo kwa uzoefu wa kazi yangu ya ualimu niliyoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, hongereni sana. Mheshimiwa Dkt. Magufuli endelea kufanya kazi, tuko nyuma yako. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kabla ya kuanza, naomba niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa hiki kibali cha kuweza kusimama kwenye Bunge lako Tukufu ili niweze kuchangia na kutoa ushauri kwenye Wizara hii muhimu sana ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambayo ndiyo mhimili wa Taifa letu kwani elimu ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu la Tanzania. Sio Tanzania tu bali nchi yoyote duniani bila elimu hakuna kitu chochote ambacho kinaweza kikafanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nitoe pongeze sana kwa Mheshimiwa Profesa Ndalichako kwa kazi nzuri, pamoja na Naibu Waziri na Katibu Mkuu na viongozi wote katika Wizara hiyo kwa kazi kubwa na nzuri ambazo wanazifanya katika kusukuma gurudumu hili la elimu katika Nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya ya kuendeleza elimu na hasa ile elimu bure. Elimu bure kwa kweli tumeweza kuona matokeo yake na matokeo yake ni pamoja na kuongezeka wanafunzi wengi sana kwenye shule zetu za msingi, hii ni kwa sababu ya elimu bure ambayo inatolewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kila mwezi zaidi ya bilioni 23 na ushehe zinatolewa kwa ajili ya kuboresha hii elimu. Mheshimiwa Rais tunampongeza sana kwa kusimamia Ilani ya Chama chetu, Chama cha Mapinduzi, chama tawala kwa kazi kubwa anayoifanya. Endelea kufanya hivi Mheshimiwa Rais, sisi tuko nyuma yako kukuunga mkono kwa Tanzania inayowezekana, kwa Tanzania mpya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alipotoa taarifa yako tumeona kuna dira, kuna dhima na kuna majukumu. Dira ya Wizara ni kuwa na Mtanzania aliyeelimika na mwenye maarifa pamoja na stadi, lakini sambamba na hilo kuna dhima; kuinua ubora wa elimu pamoja na mafunzo. Sambamba na hilo kuna majukumu; majukumu yapo jukumu la kwanza mpaka jukumu la 13, lakini la kwanza ni kutunga na kutekeleza sera, utafiti na huduma za maktaba na mambo mengine mbalimbali. Kwa kweli dira, dhima na majukumu ya Wizara yanaendana hasa na uboreshaji wa elimu hii tunayoitaka na tunayoitarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pamoja na kuwa na dira, dhima na majukumu, nataka niende kwenye eneo la Walimu wa Sayansi. Kupanga ni kuchagua, tunataka tuboreshe elimu, hatuwezi kuboresha elimu kama hatutakuwa na Walimu wa kutosha hasa Walimu wa Sayansi. Nini tunachotakiwa tufanye kwenye eneo hili; kila kitu ni maandalizi, tuliandaa Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi tukasema kwamba ifikapo mwaka 2015/2020 tunataka tununue ndege; tumenunua, tunataka tujenge reli ya kisasa; tumejenga, tunataka tuwe na vitu ambavyo vitaonekana kwa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa nini nimesema haya; kwenye hili maana yangu ni kwamba watoto wanaanza kwenye ngazi ya awali, shule za msingi, sekondari hatimaye wanakwenda kwenye elimu ya juu; naomba tuwaandae watoto hawa tangu shule za msingi, tuwaangalie kwamba watoto hawa wanataka wawe akina nani. Hili jukumu ni letu sisi kama wazazi, vilevile ni jukumu la Walimu. Walimu tuna uwezo wa kuwajua watoto hawa wanaweza kuwa ama wanasayansi au wanabiashara na fani nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tusipolianza hili mapema ni vigumu, hata tukianza kwenye level ya vyuo kama huku hatujawaandaa watoto hawa kuwa wanasayansi hatutaweza kupata Walimu waliokuwa bora wakaweza kuleta mabadiliko kwenye eneo la sayansi. Kwa hiyo, hili naomba lazima tuzingatie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapochagua wanafunzi tuweke malengo, malengo yetu ni nini; kuwapata Walimu wa sayansi. Basi tusichague tu ilimradi huyu anaweza kuwa Mwalimu, tuangalie sifa, tujipange, kama tunataka kuboresha tuangalie wa Division I, wa Division II basi hawa waende kwenye eneo la ualimu, sio wale ambao kwa kweli maksi zao haziridhishi ndiyo tunawachagua kwenda kufanya kazi ya ualimu, hili halitakuwa na tija kwetu. Ni lazima tuwekeze kwenye hili, sisi kama Serikali tuna uwezo wa kusema hili tunataka hili hatulitaki, sisi ndio wenye maamuzi, tukiwashawishi watoto hawa wanaweza kufuata kile ambacho tunakitaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyoandaa Mainjinia, tunavyoandaa Madaktari, hali kadhalika tuwaandae watoto hawa kwenda kwenye fani hiyo ya ualimu. Kwa kufanya hivyo tutapata Walimu wa Sayansi mahiri sana na hapo ndipo tutakapoweza kutafsiri dira, dhima na majukumu ya Wizara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nataka twende kwenye shule za ufundi; shule hizi ni muhimu sana kwa ustawi wa Taifa letu hasa ukizingatia kwamba tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda na tunaelekea kwenye uchumi wa kati ifikapo 2020. Hili ni muhimu kwa sababu kubwa moja; lazima tuwapate hapa mafundi wa katikati, wale mafundi mchundo, ili tuweze kuendana na hali ya sasa tuliyokuwa nayo. Kwa sababu shule zilikuwepo; kulikuwa na Tanga, Ifunda, Mtwara Technical, Dar es Salaam na zote zilikuwa zinafanya hizi kazi. Kitu kikubwa tu sasa hivi ni kufanya hayo maboresho na kurejesha hilo ili tuwe na mafundi hao wa katikati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nataka nizungumzie Bodi ya Mikopo; tunaishukuru Serikali kwa kuwashughulikia watoto yatima na wanaotoka katika mazingira magumu, watoto hawa wameweza kupata…
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Mama Salma kwa mchango mzuri.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, mengine nitayaandika. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika,asante sana. Awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kusimama. Naomba nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Waziri wa Fedha Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa uwasilishaji mzuri wa bajeti yake ya Serikali, ni bajeti yenye mwelekeo chanya kabisa kwa maslahi ya Taifa letu la Tanzania, hongera sana Mheshimiwa Mpango, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote katika Wizara hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niongelee mradi wa Rufiji Hydro Power ambao umeanza kutekelezwa tarehe 15 Juni, 2019 baada ya utekelezaji wa mambo yote ya msingi ambayo yataiwezesha kufanya shughuli vizuri katika mradi huo. Na mambo ya msingi hayo ambayo yameweza kutekelezwa ni pamoja na barabara, madaraja, kambi za wafanyakazi, maji, umeme, afya na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa utekelezaji wa mradi huu utaleta mafanikio chanya hasa ukizingatia tunaelekea kwenye uchumi wa kati, uchumi wa viwanda. Tunapoelekea kwenye uchumi wa viwanda, tunahitaji umeme wenye uhakika na umeme wenye uhakika hautapatikana katika maeneo mengine bali utapatikana kutokana na mradi huu wa Rufiji ambao mradi huu ukikamilika utazalisha megawati 2,115 na ili tuweze kuendesha viwanda vyetu hapa nchini ni lazima uwe na umeme wenye uhakika. Kwa hiyo, mradi huu umekuja wakati muafaka kwa maslahi ya Taifa letu la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kwa Serikali ni kuhakikisha mambo haya ya msingi yanafanyika. Ushiriki wa Watanzania katika ujenzi wa mradi huu, huu mradi ni mkubwa na wa kitaifa lakini pamoja na ushiriki huo, mradi huu kuna eneo maalum unatokea na eneo hilo si eneo jingine bali ni Mkoa wa Pwani katika Wilaya ya Kibiti pamoja na Rufiji. Hata kama watapewa ajira watu wengi, lakini kipaumbele nacho kizingatiwe kwa watu ambao wanatoka kwenye maeneo hayo husika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu ya pili, katika mradi huu ni lazima tuhakikishe kwamba tunahifadhi mazingira; mazingira yakihifadhiwa ndipo tutakapoweza kupata maji ya kutosha katika Mto Rufiji na ili tuhifadhi mazingira na kupata maji ya kutosha ni lazima tuweke kipaumbele katika kuhifadhi mazingira kutoka kwenye mito ifuatayo; Mto wa Kilombero, Mto wa Ruaha Mkuu pamoja na Mto wa Ruegu ambao unamwaga maji kwenye Mto Rufiji hatimaye kuelekea kwenye Bahari Kuu ya Hindi, hayo ni muhimu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la msingi ambalo nataka nilizungumzie ni nishati ya umeme maeneo ya Visiwa vya Delta. Delta ina visiwa visivyopungua 16, kwa hiyo, utakapotekelezwa mradi huu, ni lazima kuweka kipaumbele katika visiwa vile vya Delta ambavyo kuna Simbaulanga, Msufini, Sarai, Saninga na visiwa vingine vingi ambavyo vinapatikana katika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie suala la gesi; nakuja kwenye LNG ambayo inapatikana kule Likong’o katika Mkoa wa Lindi na huu ni mradi mkubwa wa kitaifa. Katika bajeti iliyopita, Waziri wa Nishati alituita tukaenda Lindi kwenye suala zima la kupata semina juu ya jambo hili, lakini amezungumza kule tulielezwa mambo mazuri, tukaelezwa mradi huu utakuwepo, tukaelezwa kwamba watu watalipwa, maeneo yale hayafanywi shughuli zozote za maendeleo hatima yake kwenye vipaumbele vya Serikali hakuna sehemu yoyote ambayo imeainishwa juu ya mradi huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Waziri Mpango, utakapokuja kufanya majumuisho, tunaomba utuambie mmefikia hatua gani juu ya mradi huu wa LNG ambao ni mradi mkubwa kwa maslahi ya Taifa letu la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumza hayo, nataka nizungumzie suala la umeme wa majumbani. Suala la umeme wa majumbani kutokana na gesi asili, tunahitaji umeme huu usambazwe kwa haraka sana katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara na Lindi kwa sababu umeme huu bei yake ni tofauti na umeme wa Gridi ya Taifa. Tunaomba hilo lifanyike na lipewe umuhimu wa kipekee kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda na tunajenga reli. Sasa reli ile inategemea chuma na hiki chuma si chuma kingine bali ni chuma cha Liganga na Mchuchuma. Hatuwezi kuelekea kwenye uchumi wa kati wakati huo tuna maliasili zilizojaa chungu nzima katika Taifa letu. Mradi wa Liganga na Mchuchuma haujapewa kabisa kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba mtakapokuja vilevile mtueleze juu ya jambo hili, tumefikia hatua gani? Ni lazima ile miradi ya kimkakati iendelezwe, siyo miradi ya kimkakati inafikia hatua inawekwa pembeni, tunamwekea nani pembeni wakati tuliipitisha sisi wenyewe? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia suala la elimu; elimu bure imeleta manufaa sana kwa Taifa hili na kwenye elimu bure tumeona kwamba wanafunzi wameongezeka kwa kiasi kikubwa sana. Sasa tunachohitaji, rai yetu; wakati wanafunzi hawa wameongezeka ni lazima waende sambamba na ongezeko la madarasa, waende sambamba na ongezeko la kuwatafuta walimu, waende sambamba na ongezeko la kuwatengenezea walimu mazingira bora zaidi. Na mazingira bora zaidi ni pamoja na kuangalia maslahi yao, kulipwa madeni yao ambayo yamerundikana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama walimu tunasema ualimu ni wito, lakini itafikia hatua – tena wengine sasa hivi wanasema ualimu kazi tu, ualimu si wito na ukimwambia, kwa mfano ukienda shuleni na nina uzoefu kama mwalimu, ukienda shuleni ukawaambia wanafunzi naomba wanafunzi nani anataka kuwa daktari utaona wananyoosha wengi sana; nani anataka kuwa engineer, wanayoosha; nani wanataka kuwa kitu gani, watanyoosha; nani wanataka kuwa walimu, huoni mtoto anayenyoosha mkono kwa sababu ya mazingira yaliyopo. Kila siku anamuona mwalimu alivyovaa, anamuona kama ni mtu dhaifu kwa vile alivyovyaa kumbe mwalimu siyo mtu dhaifu, mwalimu ndiyo anayejenga watu hawa wote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukisikia kuna madaktari, wamejengwa na mwalimu; ukisikia kuna engineer, mwalimu amefanya kazi, ukisikia kuna wanadiplomasia mwalimu amefanya kazi, ukisikia kuna wanasheria, walimu wamefanya kazi; walimu ndiyo kila kitu katika taifa hili. Kwa hiyo tunachoomba mtakapokuja hapa mtuambie mmejipangaje kuhakikisha kwamba walimu wanapata maslahi yao kwa wakati mwafaka. Ni muhimu sana katika kumjengea uwezo na yeye kujiona kwamba ni part ya wafanyakazi waliopo katika nchi hii ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, naomba tu nimalizie kwa kusema kwamba tumepewa kipaumbele kwenye kilimo, kweli kwa sababu tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda kilimo ni muhimu sana. Lakini kilimo hiki ni kilimo cha namna gani; kisiwe kilimo cha kutegemea mvua, ni lazima kiwe kilimo cha kisasa, kilimo cha umwagiliaji ndicho kitakachotutoa katika mazingira yetu haya na kuelekea uchumi huo wa kati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, ikiwezekana mia moja na zaidi. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwanza naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pili kwa sababu leo nimesimama naomba nitoe pole zangu kwa Watanzania wote kwa kumpoteza Rais wetu mpendwa, Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpe pongezi mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kushika kijiti cha kuliongoza Taifa letu la Tanzania. Sisi kama Watanzania, kama wanawake kwa ujumla tuko naye bega kwa bega kumuunga mkono Rais wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo niwape pole wananchi wangu wa Mchinga, hasa wale wa Kata ya Milola ambao wamekumbwa na kadhia ya tembo na mtu mmoja amefariki kwa kukanyagwa na tembo usiku wa jana kuamkia leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nianze kwa kuzungumzia suala la TARURA. Karibu Wabunge wote wa Bunge lako Tukufu waliosimama hapa walikuwa wanazungumzia suala la TARURA, pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri wetu na watendaji wake wameeleza vizuri sana na wao wameshika hiki kijiti vizuri sana na wao wameshika hiki kijiti.
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya Mheshimiwa wetu wa Awamu ya Sita kumuona dada yetu, mama yetu, mwanetu wetu, kwamba hapa anayefaa si mwingine bali ni Ummy Mwalimu. Naamini na najua Ummy ni mchapakazi mzuri, ni hodari na ni mfuatiliaji, ukimwomba jambo hakuna anapokuachia. Ninachopenda kusema tu TARURA inabidi iongezewe pesa. TARURA ndio kila kitu, asilimia kubwa ya wananchi wanaishi huko vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lazima tutengeneze aidha azimio kama tulivyotengeneza wakati ule kwenye eneo la maji ili tumtue mama ndoo kichwani. Tukachukua pesa kutoka eneo fulani tukasema hizi ziingizwe kwenye eneo hili ili wananchi tuwatue ndoo kichwani. Kwa hiyo ushauri wangu ili tufanikiwe kwenye hili, tunabidi tuweke hilo azimio kwamba tunataka TARURA iongezewe pesa kwa uchache hata iwe asilimia arobaini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kwenye Jimbo langu la Mchinga; Ukizunguka jimbo zima hakuna hata kipande cha sentimita moja chenye barabara ya lami. Sasa kwa misingi hii sio rahisi, halafu Jimbo lile yaani ukitoka kata moja kuelekea kata nyingine lazima upitie jimbo lingine ndipo uweze kufika. Sasa ushauri wangu na ninachoomba kwa Mheshimiwa Waziri, tuunganishiwe zile barabara zetu na TARURA, lakini kama TARURA hawajaongezewa pesa sio rahisi, siku zote zitakuwa ni barabara ambazo hazipitiki na haziunganishi hilo Jimbo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kutoka Nangalu kwenda Milola huwezi kufika kutoka Mipingo kwenda Namapwiha huwezi kufika kutoka Moka kwenda Mtumbukile ni tatizo. Naona yanakufurahisha, hayo ndio majina ya Mchinga. Kwa hiyo kule kuna changamoto kubwa zisizomithirika. (Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nataka nizungumze mradi wa EP4R. Tunaishukuru sana Serikali waliweza kutupatia hizo pesa na hata 2017/2018 walitupatia hizo pesa na walijenga mabweni mawili pamoja na vyoo, lakini mabweni yale hayajakamilika. Kuna bweni la wasichana na bweni la wavulana kwenye Shule ya Kitomanga hayajakamilika, tunaomba Mheshimiwa Waziri atuangalie kwa jicho la huruma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kibaya zaidi kama Mheshimiwa Waziri anavyojua matatizo ndani ya Mkoa wetu wa Lindi na Jimbo letu la Mchinga, wanafunzi wanasoma pale wanatoka maeneo zaidi ya kilomita 10. Hivi juzi wanafunzi wameambiwa wabaki nyumbani kwa sababu walihamia kwenye majengo ambayo yaliachwa na Wachina wakati wanajenga. Kikubwa zaidi hata Mwalimu Mkuu wa Shule ile anakaa kwenye nyumba hizo hizo ambazo zimeachwa na hao Wachina.
Mheshimwa Naibu Spika, sasa wakaguzi walipokuja wakasema nyinyi hamjajisajili kama bweni, kwa hiyo rudini nyumbani. Sasa naomba hilo nalo walitazame kwa jicho la huruma ili watoto wale waje wasome pale kwa muda, hatimaye wakitumalizia hayo mabweni, tutafanya jitihada nyingine na zilizokuwa bora zaidi sio kwamba walikaa pale kwa kupenda bali ni kwa matatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nataka nizungumzie suala la vyombo mbalimbali ambavyo Mwalimu anaitika; vyombo hivi ni vingi kuna TAMISEMI, Wizara ya Elimu, TSC - Tume ya Utumishi wa Walimu na sasa kuna chombo kingine kinachokuja kinaitwa Bodi ya Kitaalam ya Mwalimu. Sasa hivi vyombo ni vingi, Walimu wenzangu wameniagiza kwa sababu mimi kwa taaluma ni Mwalimu, wanachohitaji hapa wabaki na chombo hiki kimoja wabaki ambacho ni TSC na sio Bodi ya Kitaaluma ya Mwalimu. Wanahitaji hivyo kwa sababu TSC inahudumiwa na Serikali, lakini hiki chombo kikishaundwa na Serikali anatakiwa Mwalimu huyu mwenyewe akiendeshe na ni ngumu sana ukizingatia hata hali yenyewe ya Mwalimu nayo ni mtihani kwake. Tunaomba waliangalie hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nataka nizungumzie Walimu kutopandishwa madaraja kwa wakati na kutorekebishiwa mishahara yao kwa wakati. Naomba hili jambo waliangalie kwa utete wake ili Walimu wapandishwe madaraja yao kwa wakati na warekebeshiwe. Kwa mfano, kuna Walimu wa 2014/2015, hawa hawa hawajapanda kabisa madaraja na hata wale wa mwisho kupanda madaraja 2014 imekuwa mwisho. Naomba Serikali waliangalie hilo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa kwa unyenyekevu wake mkubwa utupe jibu sahihi kuhusu TSC na atupe jibu sahihi kuhusu hiyo Bodi kwani hawaitaki kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nikushukuru sana kwa kunipa fursa, nitasubiri Wizara nyingine ili niweze kuchangia hoja zangu Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru, sambamba na hilo nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehma na Utukufu kwa kutujaalia uzima na uhai. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mwezi Mtukufu wa Ramadhan niwapongeze Watanzania na Waislam wote ulimwenguni kwa kukaribia kumaliza mwezi huu Mtukufu wa Ramadhan. Tunawatakia kila la kheri na mafanikio makubwa kuelekea kwenye Eid El-fitri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeza wizara kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya katika kuboresha suala zima la elimu yetu ya Tanzania. Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kila bajeti lazima watenge mafungu kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu pamoja na kutoa nafasi za ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba miundombinu imeboreshwa lakini kuna changamoto nyingi katika miundombinu hii ikiwepo suala zima la maabara, madarasa, vyoo vya walimu, vyoo vya wanafunzi na miundombinu mingine mbalimbali na hasa nyumba za walimu. Changamoto hizi haina maana kwamba hakuna kilichofanyika kuna mambo mengi na makubwa yamefanyika lakini hakuna mambo utakayoweza kuyamaliza kwa wakati mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu ni msingi wa kila kitu katika maisha ya mwanadamu. Mwanadamu asipokuwa na elimu kwa kweli anakuwa yupo nyuma. Nikirejea kwa Nabii wetu Muhammad (S.A.W) alipopewa Utume, alisema mimi siwezi kusoma. Mwenyezi Mungu akamwambia usiwe na wasiwasi kwa sababu alipewa ule Utume ili awaongoze Waislam au wafuasi wake. Mwenyezi Mungu akamteremshia Sura inaitwa Iqra bismi rab bikal lazee khalaq kwamba nenda kasome na alipomwambia asome hakumwambia asome kitu kimoja, alimwambia soma mpaka China. Leo China ni nchi inayoongoza kwa sayansi na teknolojia katika ulimwengu huu wa leo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nini mantiki ya kuyasema haya. Tunaboresha elimu yetu kama Nabii Muhammad asingekuwa na walimu wa kumfundisha asingeweza kupata mafanikio makubwa. Sasa kwa mukhtadha huu nataka nichangie kuhusu udhibiti wa elimu na upungufu wa walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukianzia kwenye suala la walimu. Tunampongeza Mheshimiwa Waziri wetu Profesa Ndalichako pamoja na timu yake ya wataalam na wametuambia kwamba kuna mkakati madhubuti wa kuongeza walimu katika nchi yetu ya Tanzania yaani kutoa vibali kwa ajili ya ajira na vibali 6,000 vitatolewa. Sasa vibali 6,000 vikitolewa maana yake ni nini? Tuna walimu 6,000, tuna halmashauri 185, kwa uwiano ina maana kila halmashauri itapata walimu 32.43. Walimu hawa kwa kweli ni wachache sana ukilinganisha na uhaba wa walimu tuliokuwa nao. Ushauri wangu hapa ni nini? Ni lazima tuongeze walimu wengi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada kuyasema hayo, nikubaliane na Kamati yangu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusiana na changamoto zilizopo. Niongelee Udhibiti wa Ubora. Hiki chombo ni muhimu sana tena sana ni sawasawa na Taasisi ya CAG. CAG bila kuwepo ina maana kwamba upungufu mwingi uliojitokeza katika maeneo mbalimbali usingeweza kuonekana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu kazi yake ni kuandaa somo na kulifundisha. Lazima awe na Scheme of Work na Lesson Plan. Akishafundisha atajitathmini yeye mwenyewe. Sasa pamoja na kujitathmini yeye mwenyewe, hatutaweza kuboresha elimu kama hakutakuwa na wadhibiti ubora ambao watakuwa wanapita shule nyingi mbalimbali hapa nchini kuona je, alichokiandika huyu mwalimu na jioni akakitathmini ni sahihi? Maana huwezi kuandika kitabu ukakihariri wewe mwenyewe na ukahariri mara ya kwanza, ya pili na ya tatu. Kwa hiyo, mwalimu huyu anatakiwa awe na hiki chombo ili ajione kile alichokifanya ni sahihi au siyo sahihi? Kiko sawa au hakiko sawa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mdhibiti ubora ili aweze kufanya kazi yake vizuri zaidi ni lazima awe na vitendea kazi. Awe na bajeti inayojitosheleza. Akiwa na bajeti hiyo, ina maana kwamba atafanya kazi yake kwa umakini zaidi na kuhakikisha kwamba shughuli inakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye uhaba wa walimu, kwa mfano, ukienda kwenye jimbo langu la Mchinga peke yake, tuna uhaba wa walimu chungu nzima. Ninachoshauri, walimu hawa wanapopangwa vile vile tuwapange walimu wa kike. Kwa mfano, shule yangu ya Nangaru haina mwalimu wa kike hata mmoja. Binti akiingia kwenye ule mfumo wake wa kwenda kule angani, au ndiyo imeingia sasa hivi, anaongea na nani? Kwa hiyo, tunapopanga tuhakikishe kwamba walimu wa kike wanapewa nafasi kwenye shule zetu nyingi zilizopo hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenda angani, maana yake kuwa katika kipindi cha hedhi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Naomba nianze kwa kumshukuru Mungu. Hatimaye nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa uwasilishaji wake mzuri ambao umegusa sehemu nyingi katika eneo lake la Wizara yake, vile vile nawapongeza wataalam kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nijikite katika mambo machache sana, kwanza kuhusiana na suala zima la barabara. Kama mnavyofahamu na mnavyojua barabara ya kuelekea kusini inaanzia Kilwa inaishia Mtwara lakini katikati hapa kuna sehemu inaitwa Mingoyo. Hii barabara ni barabara ya Taifa na hii barabara iko chini ya TANROAD, lakini barabara hii sidhani kama kuna barabara inayofanana nayo katika nchi hii kwa upungufu wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa mvua barabara hii imeharibika sana tena sana. Ninachoomba na ninachoshauri pamoja na kwamba Mheshimiwa Dkt. Pombe Joseph Magufuli, Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema, alipokuja kwenye mbio za kuzima mwenge kitaifa ilifanyika kule, alisimama pale njiani na akatoa order na ile order ilitekelezwa kwa kile kipande. Tunashukuru imemalizika, lakini sehemu kubwa barabara hii sio nzuri na wala sio salama na inapitiwa na magari mengi na mazito.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, katika bajeti haipo, sikuiona sehemu yoyote barabara hii. Lindi - Dar es Salaam ni sawa na sehemu nyingine yoyote katika Taifa hili la Tanzania. Naomba waiwekee bajeti ili barabara hii nayo itengenezwe, maeneo mengi ya barabara hii ni mabovu. Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ninalotaka niliombe kwa ujumla wake naongelea Jimbo la Mchinga ambalo ndio Jimbo langu. Katika jimbo hili kuna sehemu inaitwa Mchinga A na Mchinga B au Mchinga I na Mchinga II. Pale kuna wanafunzi wanaotoka Mchinga I kuelekea Mchinga II, wanafunzi wale wanapata adha kubwa ya kuvuka kwa miguu na yale maji ni mengi, pale kuna mkondo wa bahari maji yale ni mengi sana. Watoto wengi na watu wazima wamepoteza maisha yao kwenye eneo lile.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye ujenzi wa madaraja pamoja na ujenzi wa maboti na kuwapatia watu maboti, kwenye eneo hilo naamini tutapata usafiri kwa ajili ya kuwanusuru wanafunzi wale ili wasiweze kufa wakati wanavuka pale kwenda Mchinga II kutafuta elimu yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini elimu ni haki ya msingi kwa kila mtu, nilisema Jimbo la Mchinga ni Jimbo pekee ambalo halina barabara ya lami hata kidogo, wengine wanasema tuna nusu kilomita, wengine kilometa moja, wengine sijui kilometa 10, lakini Mchinga hakuna, labda lami utaiona pale sehemu inayoitwa Rutamba kuelekea Rondo na ile nafikiri ni private haikuwekwa na Serikali
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba hili Jimbo la Mchinga nalo wale watu wanataka waione hiyo lami sasa lini watatuwekea hiyo lami. Naomba tufanye hima hata kidogo tupate, Jimbo la Mchinga ni Jimbo gumu, Jimbo la Mchinga linataka lifunguliwe, Jimbo la Mchinga linazalisha mazao mengi ya chakula na biashara, korosho zinatoka Mchinga, ufuta unatoka Mchinga, tuna kila sababu ya kuiangalia Mchinga kwa jicho la aina yake.
Mheshimiwa Naibuu Spika, nilisema nitasema machache tu, baada ya kusema hayo, nimalizie kwa kusema, naomba Waziri atakapokuja kufanya majumuisho, basi mtupatie angalau majibu ya matumaini kwa Jimbo letu la Mchinga na Wanamchinga.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana na nawatakia Wizara kila la heri. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu kwa ustawi wa Taifa letu la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha hoja yake kwa umahiri mkubwa. Sambamba na hilo niwapongeze wasaidizi wote ambao wameifanya hii kazi na ikawa nzuri. (Makofi)
Sasa mimi nataka kuchangia katika maeneo makubwa mawili; eneo la kwanza la michezo na eneo la pili ni kuhusiana na suala zima la lugha ya Kiswahili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nikianzia na michezo, Wabunge wengi na kila Mbunge ambaye amesimama hapa anazungumzia suala zima la michezo na lazima tukubali kwamba michezo ndiyo inayowapa raha Watanzania na ndiyo inayowapa raha watu mbalimbali duniani kote. Kila aliyesimama hapa amezungumzia Simba na Yanga. Hata humu kwenye Bunge letu hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, timu kubwa ambazo tunazungumzia, zinazungumziwa kama sio Simba, itazungumziwa timu ya Yanga. Kwa hiyo, niwapongezeni sana, tena sana kwa hoja nzito ambazo mmezitanguliza kuzitoa. Tunafarijika sana Watanzania hasa Yanga na Simba zinapoingia uwanjani. Hatimaye mmoja akashindwa na mmoja akashinda au mmoja akashinda na mwingine akashindwa, lakini baada ya hapo tunakuwa kitu kimoja udugu wetu unaendelea kustawi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa nizungumzie suala la michezo kwenye suala la vifaa na wataalam. Tunajua kwamba kuna kitu kinaitwa UMISETA na kuna kitu kinaitwa UMITASHUMTA. Sasa tukianzia na UMITASHUMTA, ni ngazi ya mwanzo kabisa kule kwenye shule za msingi hasa zile shule zetu za awali. Sasa tukienda kule kitu ambacho ni changamoto kubwa ni vifaa, vifaa kule hakuna. Hakuna mipira, hakuna mikuki kwa ajili ya kurusha, hakuna visahani kwa ajili ya kutupa, hata viwanja vyenyewe ni mtihani mkubwa sana kwenye eneo la michezo. Kitu kikubwa na cha kushangaza mpira wa miguu ndiyo mpira unaopendwa, ukienda kwenye zile shule hata magoli hakuna. Ukienda wewe kama Mbunge unaambiwa sasa Mbunge tuletee magoli, Mbunge tuletee mipira, sasa mipira hiyo hata ukipeleka, magoli hakuna. Wanacheza nini? Hakuna cha kucheza. (Makofi)
Kwa hiyo, kwenye bajeti hii ambayo imeidhinishwa, kwa ushauri wangu ni lazima tuangalie kwenye shule zetu za msingi na za sekondari kupeleka mipira pamoja na vifaa vingine vitakavyowasaidia watoto au wanafunzi kucheza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hiyo ukiachana na vifaa vya michezo wa mpira, hakuna wataalam. Kwenye shule zile za msingi hata sekondari hakuna hata mwalimu wa michezo, yaani mwalimu tu mtafute huko mtaani au wapi sijui ndipo aende. Tunazungumzia leo timu ya Taifa, kama wale wasingekuwa na wataalam, hiyo timu ya Taifa ingeweza kupatikana? Au timu ya Yanga isingekuwa na wataalam wangefikia pale walipofikia? Au timu yetu ya Simba isingekuwa na wataalam wangefikia pale walipofikia? Isingewezekana! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukitaka kujenga kitu, anzia kwenye ngazo ya shina kule. Hata Cchama chetu cha Mapinduzi watu wako shinani kule mpaka huko Taifani. Sasa tuanze kwenye shina kule kujenga hii michezo ili tuibue vipaji kwa ajili ya watoto hawa waendelee mbele ya safari. Hili ni muhimu sana katika ustawi wa michezo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa baada ya kuchangia kwenye hilo eneo la michezo nataka nizungumzie kwenye suala la lugha. Tulizungumza hapa, lugha ni sauti za nasibu zinazobeba maana na zilizokubaliwa na jamii ya watu ili zitumike katika mawasiliano. Kwenye lugha hakuna lugha iliyokuwa bora zaidi ya lugha nyingine, isipokuwa lugha huongeza msamiati wake. Lugha inakua na lugha inakufa, kufa kwa lugha ni kwa kutotumiwa na watu wengi duniani na kupunguza msamiati wake. (Makofi)
Leo tukizungumzia suala la Kiingereza, sio lugha bora kulikoni lugha ya Kiswahili isipokuwa watu wengi wanazungumza. Tukizungumzia hali kadhalika Kifaransa, Kifaransa sio bora kuliko lugha nyingine isipokuwa Kiswahili chetu ni lugha bora na ziliwekwa hizo lugha kwa sababu ya kututawala. Sasa kama tuna lugha yetu kwa nini tusiitumie hiyo lugha yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni muhimu kutumia lugha ya Kiswahili na tujisikie tuna raha, amani kwamba tuna lugha yetu ambayo itazungumzwa ndani ya Bara letu la Afrika na watumiaji wa lugha hii ni wengi kweli. Siku hadi siku wanaongezeka duniani kote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa kwa mantiki hiyo au kwa muktadha huo kuna suala la wakalimani. Tumemsikia Mheshimiwa Waziri hapa anatueleza, wakalimani waliopo wote jumla yake ni 45 tu na kati ya 45 hao 20 ndiyo wataalam, 25 wanahitaji usaidizi. Kwenye eneo hili ni lazima tutengeneze mkakati muhimu kuhakikisha kwamba wakalimani hawa wanaongezwa. Kwa mfano leo, Afrika nzima ikisema tunahitaji wakalimani wawili kila nchi, au hata mmoja tu ina maana kwamba hatuwezi kutosheleza mahitaji ya wakalimani kwa sababu tuna nchi zaidi ya 56 na wakalimani waliopo ni 45. Tutafika kweli? Lugha ni biashara, wakalimani hawa ni biashara. (Makofi)
Kwa hiyo, tukiongeza wakalimani bado tutaongeza fursa ya biashara ndani ya lugha yetu ya Kiswahili. Naomba hili lizingatiwe kwa umakini mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, la mwisho, nimesema nitachangia katika maeneo mawili tu wala sio mengi; la mwisho, kama tunavyofahamu na tunavyotambua Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli alisisitiza sana suala la lugha na sasahivi tunae Mama Samia Suluhu Hassan.
Ninachoomba na kushauri, katika wasaidizi wake, Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan kuwe na msaidizi maalum wa lugha ya Kiswahili kama walivyo washauri wengine katika eneo la siasa, uchumi na maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia Wizara hii ambayo ni Wizara muhimu sana katika ustawi wa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda nimpongeze Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya ndani ya Taifa letu na nje ya mipaka yake. Leo hii dunia yote inatambua kwamba Rais wa Tanzania yupo na anautangaza utalii wa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, niipongeze Wizara ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora ambayo inaongozwa na Dada yetu mpendwa Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa kweli anafanyakazi nzuri, kazi hii anayoifanya si kwamba ameanzia hapa bali ameanzia kwenye maeneo yote ambayo alikabidhiwa dhamana ya kushughulikia shughuli hizo. Hongera sana Mheshimiwa Mama Jenista Mhagama, endelea kufanya hivyo Taifa linakutegema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo napenda nichangie kwenye eneo la watumishi tu. Eneo hili ni eneo muhimu. Kwanza, naungana na wenzangu wote, Waheshimiwa wote ambao wamechangia eneo hili kwa kuona na kutambua kwamba mtumishi ana haki yake ya msingi amefanya kazi kwa wakati wake, na anapostaafu anatakiwa atambuliwe kwamba alichangia Taifa hili katika eneo moja au jingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo leo hii kwanza mimi namshukuru Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa nini namshukuru kwa sababu yeye aliniteua kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia vile viti 10. Kutokana na hilo leo hii naweza kusimama hapa na kuzieleza changamoto, hapa nataka nieleze wastaafu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wastaafu hawa wapo katika eneo maalum ambao ni Wenza wa Viongozi. Wake wa Marais, Wake wa Mawaziri Wakuu na wake wa Makamu wa Rais. Ninayaeleza haya kwa sababu na mimi nataka niseme nilikuwa ni Mke wa Rais wa Awamu wa Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu na suala la kustaafu mara Rais anapochaguliwa ili aweze kushika kijiti na kuongoza Taifa. Mke wa Rais anatakiwa astaafu asiendelee kufanyakazi, hatakaa kana kwamba alikuwa ni mtumishi wa umma, unatakiwa kuanzia wakati ule ustaafu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mfano mmojawapo nilitakiwa niache kazi yangu ya Ualimu niendelee na shughuli nyingine. Sasa kwa muktadha huu kuacha kazi siyo jambo baya lakini kinachotakiwa kifanyike ajue huyu Mke wa Rais au Mke wa Makamu au Mke wa Waziri Mkuu stahiki zake zipo wapi? Stahiki zake ni nini mara baada ya kustaafu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama akistaafu ni lazima huyu Mke wa Rais basi apate mafao yake yale mapema au haraka kadri inavyowezekana. Sasa itokee Mke Rais huyu, kama huwiwi ina maana kwamba kuanzia siku ile inabidi ukae nyumbani uendelee na shughuli za nyumbani wakati wewe ulikuwa aidha mtalaam kwenye eneo husika, kwa maana hiyo utaalam wako wote ule unatoweka na inakuwa basi, ukiwiwa sana ndiyo unaweza ukasema hebu nianzishe NGO. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukianzisha NGO ile hakuna mtu anayeku-support, ni wewe mwenyewe binafsi uhangaike kona zote, kuhakikisha kwamba unapata rasilimali ili uweze kuendesha ile NGO. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu au ushauri wangu, tengenezeni utaratibu maalum wa kisheria kwamba, huyu Mke wa Rais mara au mwenza kwa mfano leo si mke wa Rais leo ni mwenza Mama leo ndiyo Rais, Baba ndiyo mwenza wake huyu Baba ina maana anaachishwa kazi leo na akiachishwa kazi anafanya nini? Tengenezeni yale mazingira mazuri ili tunapomaliza ule muda tujue tuna kitu gani ambacho tunatakiwa tukifanye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Ofisi ya Rais, Utawala Bora ni imani yangu kwamba, tutatengeneza utaratibu au sheria inayomuhusu mke wa Rais au wenza nini baada ya hapo kiendelee kufanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo muhimu sana siyo kwangu mimi bali ni kwa vizazi vijavyo na vijavyo kujua stahiki zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ahsante sana Mheshimiwa Mama Jenista Mhagama kwa kazi kubwa na nzuri unayoifanya Mwenyezi Mungu akubariki, Mwenyezi Mungu ambariki Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kazi iendelee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia kwenye Wizara ya Maji.
Awali ya yote naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa Wizara ya Maji kwa Mheshimiwa Waziri wa Maji pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu na Wizara kwa ujumla kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Sambamba na hilo nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuwatua wanawake ndoo kichwani. Ama kweli hakuna mwanamke anayeweza kutupa mtoto wake, na mama ametambua tatizo la maji ni tatizo la wanawake. Tuna mpongeza sana.
Mheshimiwa Spika, nilisimama kwenye Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwaajili ya kuomba maji na Mheshimiwa Waziri akanihakikishia na akaniambia; ukiona mama mtu mzima analia ujue kuna jambo; nitahakikisha hili jambo linamalizika au kupungua kwa kiasi kikubwa; na ndiyo maana leo nimesimama kwa ajili ya shukran. Mheshimiwa Waziri amenipatia pesa takriban bilioni 12.5 kwa ajili ya mradi mkubwa kutoka chanzo cha Ng’apa kuja Mitwero hatimaye kusambaza mabomba katika Jimbo letu la Mchinga, ahsante sana Mheshimiwa Waziri kwa fedha hizo ambazo umenipatia. Sasa ninaamini lile tatizo la maji limeanza kupungua na baada ya muda si mrefu tatizo la maji litatoweka katika Jimbo letu la Mchinga ambalo liko katika Manispaa ya Lindi.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo kuna Tarafa ya Mipingo tayari maji sasa hivi yanatiririka. Mheshimiwa Waziri wanakusubiri tu uje uzindue kama ambavyo ulivyoahidi wakati ule tulipokuwa pale Mnyangara ahsante sana Mheshimiwa Waziri. Haukuishia hapo tatizo la maji la Mchinga lilikuwa ni tatizo tete na ni tatizo kubwa; maji kulikuwa hakuna walikuwa hawajui maji ya bomba sasa hivi maji yanatiririka bombani.
Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo ukanipatia visima vinne na tayari hivyo visima vinne vimeshakuwa katika harakati za kumalizika kuna kisima cha Kilolambwani tayari kimemalizika, Uleka kule kisima kimemalizika na maji yanabubujika hayana hata utaratibu jinsi yanavyobubujika ahsante sana. Sasa tuko kwenye kisima kile cha tatu Namkongo ambako Namkongo kulikuwa na shida kubwa ya maji; wakitoka Namkongo wanamalizia Nanjime. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kunipatia maji katika Jimbo langu la Mchinga.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, kuna bilioni 1.5, na hii umetupelekea Mnyangara na tayari kazi inafanyika; umetupelekea Mputwa tayari kazi inafanyika; vile vile umetupelekea Kiwawa kazi zinafanyika, na ndiyo maana nimesema nasimama hapa kwa ajili ya kutoa shukrani zangu za dhati kwa kazi kubwa na nzuri ambayo imefanyika. Mwaka 2022/2023 bado kuna miradi mipya ambayo mmetupatia.
Mheshimiwa Spika, kuna mradi mpya wa upanuzi kutoka Kilangala kwenda Mihambwe Sinde hatimaye kufika kule Mtumbikile. Mradi huu una jumla ya shilingi milioni 340. Sambamba na hiyo kuna mradi ambao utakuwa ni Phase II kutoka Moka kwenda Matimba; na maeneo haya yote yalikuwa na matatizo makubwa ya maji huku umetupatia milioni 250 jumla ya milioni 590. Hukutuacha hapo hivyo hivyo bado ukatupatia visima vitano ambavyo vitachimbwa katika Jimbo letu la Mchinga. Nasema ahsante sana.
Mheshimiwa Spika, kila kwenye mafanikio hapakosi kuwa na changamoto. Sambamba na mafanikio hayo makubwa ambayo tumeyapata kwa muda mfupi katika Jimbo letu la Mchinga bado tuna changamoto katika tarafa ya Milola kuhusiana na suala la ukarabati na mabomba ambayo ni chakavu katika ile kata ya Milola. Maji yapo lakini yanayomwagika ni mengi sana. Tunachoomba Mheshimiwa Waziri utusaidie kiasi cha fedha ili tuweze kufanya ukarabati wa mabomba yale ambayo yanavujisha maji kutoka kwenye chanzo hadi kwenye bomba kuu pale Nyirola.
Mheshimiwa Spika, ushauri mwingine ambao nashauri huu mradi ambao ni wa bilioni 12.5 pesa ambazo tayari zimetoka ni bilioni 1.8 na ni mradi wa mwaka mmoja. Ombi langu kwa Serikali ombi langu kwako Mheshimiwa Waziri mtufanyie kadri inavyowezekana kadri bajeti inavyoruhusu ili kutupatia zile pesa kwa wakati ili ifikapo tarehe 3 Mei, 2023 kama tulivyokubaliana mradi huu uwe umekamilika. Tulikubaliana kwenda kusaini ule mkataba na ulikuwa tayari. Mheshimiwa Waziri vile vile nitakuomba twende tukazindue ule mradi wakati huo huo kazi iendelee.
Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. ninaipongeza sana kwa kazi kubwa na nzuri ambayo unaifanya. Ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kutupatia na kwa kuwatua ndoo wanawake wa Jimbo la Mchinga. Mwenyezi Mungu akubariki Mwenyezi Mungu awabariki. (Makofi)
SPIKA: Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete kabla hujakaa tusaidie Jimbo la Mchinga liko Mkoa gani hapa nchini? Washa kisemeo chako.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Mchinga lipo Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Lindi ndiyo mkoa ambao Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anatokea huko katika Jimbo la Ruangwa. (Makofi)