Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi (22 total)

MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y. MHE. RITTA E.
KABATI) aliuliza:-
Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 imekuwa ya muda mrefu na hivyo kupitwa na wakati.
Je, ni lini sheria hii itafanyiwa marekebisho ili iendane na mahitaji na kuondoa upungufu uliopo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ni matokeo ya mjadala mpana na shirikishi kupitia Waraka wa Serikali Na.1 ya mwaka 1969. Lengo la mjadala huo lilikuwa kupata muafaka kuhusu maudhui ya sheria hiyo ambayo yaligusa imani, mila na desturi za Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya miaka zaidi ya 20 kupita tangu Sheria hiyo ya Ndoa itungwe, Serikali kupitia Tume ya Kurekebisha Sheria iliifanyia mapitio sheria hiyo na kubaini maeneo kadhaa yenye udhaifu na hivyo kuhitaji kufanyiwa marekebisho.
Mheshimiwa mwenyekiti, kutokana na maoni hayo ya tume, mwaka 2008 Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria iliandaa Waraka wa Baraza la Mawaziri uliokuwa na mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Ndoa ya M waka 1971.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mnamo Desemba, 2010 kabla ya waraka huo kujadiliwa na kuridhiwa na Baraza la Mawaziri, mchakato wa mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukaanza na kulilazimu baraza kusitisha kwa muda mchakato wa marekebisho ya Sheria ya Ndoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilikuwa na matarajio kuwa wakati Tume ya Mabadiliko ya Katiba inakusanya maoni ya wananchi kuhusu mabadiliko ya Katiba, wananchi wangetoa maoni kuhusu Sheria ya Ndoa pamoja na sheria nyingine zinazofanana na hiyo. Hata hivyo, maoni yaliyotolewa wakati wa mchakato huo kuhusu Sheria ya Ndoa yalikuwa machache sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na muda kupita na mabadiliko kadhaa yaliyotokea kuhusu Sheria ya Ndoa, Wizara yangu imeendelea na mchakato wa ndani wa kuifanyia mapendekezo ya marekebisho sheria hiyo. Wakati muafaka utakapofika, tutawasilisha mapendekezo ya
marekebisho ya sheria hiyo Bungeni ili iweze kuendana na wakati kwa kuondoa upungufu uliopo kwa maslahi mapana ya nchi yetu na kuhuisha na kuimarisha maeneo yaliyo mazuri ndani ya sheria hiyo.
MHE. SALEH ALLY SALEH (K.n.y. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED) Aliuliza:- Kwa kipindi kirefu sasa kumekuwa na matendo ya dhahiri yanayoonesha kuvunjwa kwa haki za binadamu hapa nchini bila ya Serikali kuchukua hatua yoyote.
Je, Serikali haioni kwamba wananchi watakosa imani na Serikali yao?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Muhammed Amour Muhammed, Mbunge wa Bumbwini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya jukumu la msingi kwa Serikali ni kukuza, kulinda na kuhifadhi haki za binadamu na wajibu wao hapa nchini. Jukumu hilo ni la kikatiba ambapo Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, kama ilivyorekebishwa mara kwa mara na Katiba ya Zanzibar ya 1984 kama ilivyorekebishwa mara kwa mara pamoja na kuainisha haki za binadamu, imeipa Serikali wajibu wa kukuza, kulinda na kuhifadhi haki hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia Bunge lako Tukufu, nchi yetu imeridhia mikataba mbalimbali ya Kimataifa na kikanda ambayo inaweka misingi ya haki hizo na wajibu wa Serikali katika kuhakikisha nchi inaendeshwa kwa kufuata misingi ya haki za binadamu. Aidha, Bunge lako Tukufu kwa nyakati tofauti limetunga sheria mbalimbali zinazolinda na kukuza haki za binadamu pamoja na kutoa nafuu (remedy) kwa raia pale haki za binadamu zinapovunjwaaidha na Serikali au mtu binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa, zinadumishwa na zinastawishwa hapa nchini, Katiba imeipa Mahakama mamlaka ya kusikiliza na kuamua mashauri yanayohusu haki za binadamu na wajibu wao kama ulivyoainishwa katika Katiba. Aidha, Serikali imeunda taasisi mbalimbali zinazoshughulikia hifadhi ya haki za binadamu. Taasisi hizo ni pamoja na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na Mabaraza mbalimbali kama yale ya Ardhi na Kodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama pamoja na taasisi hizi zimekuwa zikichukua hatua pindi vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu vinapotokea na kuripotiwa au kufikishwa kwa maamuzi. Serikali kupitia vyombo vyake, imejidhatiti kuhakikisha kuwa kitendo chochote kinachovunja haki za binadamu kinachukulia hatua stahiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwasihi Waheshimiwa Wabunge tushirikiane na vyombo vyetu vilivyopewa mamlaka na dhamana ya kulinda haki pale tunapopata taarifa za vitendo vya uvunjwaji wa haki za binadamu vimefanyika au vinaweza kufanyika ili hatua stahikina za haraka za kisheria zichukuliwe.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO Aliuliza:-
Katika miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia baadhi ya sheria zetu hapa nchini kutoendana na mabadiliko na kasi ya maendeleo ya Taifa na kuonekana kuwa zimepitwa na wakati.
Je, ni lini Serikali italeta hoja ya kufanya marekebisho ya kuboresha baadhi ya sheria zilzopitwa na wakati?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Phillipo Augustino Mulugo, Mbunge wa Songwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia kupitia Wizara mbalimbali imekuwa ikiwasilisha Miswada ya Sheria mbalimbali Bungeni kwa lengo la kuhakikisha Taifa linakuwa na Sheria zinazochochea ukuaji wa uchumi, uboreshaji wa huduma na ustawi wa jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali pia kupitia Bunge lako Tukufu imekuwa ikifanya marekebisho ya Sheria Mbalimbali ili ziendane na wakati kupitia Miswada ya Sheriaya Marekebisho Mbalimbali (Written Law Miscellaneous Amendments).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kuboresha sheria ni endelevu katika kuhakikisha sheria zetu zinaendana na mabadiliko yanayotokea katika jamii na kwa hiyo, Serikali itaendelea na utaratibu uliopo wa kuhakikisha kuwa sheria za nchi zinaendana na wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria za nchi hubadilika kulingana na mabadiliko ya kijamii, kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni, kisayansi na kiteknolojia. Mabadiliko yanapojitokeza, yanaweza kuathiri sheria zilizopo na hivyo kuonekana kuwa zimepitwa na wakati au kuwa na upungufu hivyo kutokidhi matakwa ya wakati. Hali hii hulazimu kufanyika kwa marekebisho ya sheria husika ili kuendana na wakati kulingana na mabadiliko yaliyotokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia ukweli huo, mwaka 1980 Serikali iliunda Tume ya Kurekebisha Sheria kama chombo maalum chenye dhamana ya kuzifanyia mapitio Sheria zilizopo ili kukidhi malengo na makusudio ya kutungwa kwake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani miaka 37 sasa tangu kuundwa kwa Tume ya Kurekebisha Sheria, imekuwa ikifanya tafiti mbalimbali za sheria na kupendekeza maboresho pale inapoonekana kuna umuhimu wa kufanya hivyo. Maboresho hayo yanaweza kupelekea kufutwa, kutungwa upya au kufanyiwa marekebisho sheria iliyopo ili kuendana na wakati uliopo.
MHE. ISSA A. MANGUNGU aliuliza:-
Wazee wa Mabaraza katika Mahakama Kuu hasa Dar es Salaam husikiliza kesi zinazohusu mauaji na kulipwa sh. 5,000:-
Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kuwaongezea posho wazee hao?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mchango mkubwa wa Wazee wa Baraza katika Mahakama zetu na umuhimu wa kutoa posho kama motisha. Kutokana na umuhimu huo, Serikali ingetamani sana posho za wazee hao ziongezeke ili kuendana na hali ya uchumi, lakini kwa bahati mbaya posho hizo hutokana na bajeti ya matumizi mengineyo (other charges) ambazo hutengwa na Serikali kwa kila fungu.
Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017, Mahakama ya Tanzania ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 1.27 na mwaka 2017/2018, Mahakama imetenga shilingi bilioni 1.85 kwa ajili ya malipo ya posho ya wazee wa Baraza. Fedha kwa ajili ya Wazee wa Baraza ni fedha zinazotengwa katika eneo la matumizi ya kawaida, hivyo Serikali kupitia Mahakama itaendelea kutenga au kuongeza posho kwa malipo mbalimbali zikiwemo posho kwa ajili ya Wazee wa Baraza.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala kwamba Wazee wa Mahakama wataongezewa posho zao kwa kadri bajeti itakavyokuwa inapatikana.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Katika Jimbo zima la Mlimba hakuna Mahakama hata moja, jambo linalosababisha mahabusu kupelekwa Jimbo la Kilombero umbali wa takriban kilometa 260 kuhudhuria mahakama:-
Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama katika Jimbo la Mlimba ili kuwaondolea wananchi adha ya kusafiri umbali mrefu katafuta huduma ya Mahakama?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suzan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, uanzishaji wa Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo nchini unaongozwa na Sheria ya Mahakimu, Sura 11 ya Sheria za Tanzania (The Magistrate Courts Act, Cap. 11) of the laws of Tanzania. Kifungu cha 3(1) kinaeleza kuwa katika kila Wilaya kutaanzishwa Mahakama za Mwanzo; Kifungu cha 4(1) kinaeleza kuwa kutaanzishwa Mahakama za Wilaya katika kila Wilaya na Kifungu cha 5(1) kinampa mamlaka Jaji Mkuu kutoa amri ya kuanzisha Mahakama za Hakimu Mkazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Mlimba, Tarafa ya Mlimba ipo Mahakama ya Mwanzo inayoendelea kutoa huduma hadi hivi sasa. Serikali inatambua kuwa miundombinu ya Mahakama hiyo hairidhishi na hivyo katika mwaka wa fedha 2017/2018 tumepanga kujenga Mahakama ya Mwanzo mpya katika Tarafa ya Mlimba.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umbali na ukubwa wa Wilaya ya Kilombero yenye Majimbo ya Kilombero na Mlimba na itajitahidi kuhakikisha kwa kadri ya uwezo utakavyokuwa kujenga Mahakama za Mwanzo za kutosha katika Wilaya nzima ya Kilombero ili kusogeza huduma za Mahakama na utoaji haki karibu zaidi na wananchi.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya ya Chunya.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA K.n.y WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, Mbunge wa Lupa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Chunya ni moja ya Wilaya za zamani ambazo mpaka sasa hazina majengo kwa ajili ya Mahakama ya Wilaya. Kwa sasa Mahakama inendeshwa katika majengo ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na nafasi ndogo sana kukidhi matumizi ya huduma za Mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mkakati wa maboresho ya huduma za Mahakama tumepanga kujenga jengo la Mahakama ya Wilaya ya Chunya katika mwaka huu wa fedha, 2017/2018. Hivyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Chunya kuwa na subira, wakati mipango inafanyika ya kujenga Mahakama hiyo.
MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-
Je, ni lini Mahakama zote nchini zitaanza kuendesha kesi kwa lugha ya Kiswahili?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI NA MICHEZO (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 12 cha Sheria ya Mahakama Sura ya 11 yaani (Magistrates’ Courts Act CAP 11; S.12), lugha inayotumika kuendesha kesi katika Mahakama zote za Mwanzo ni Kiswahili. Aidha, kifungu hiki kinatamka kwamba kesi katika Mahakama za Wilaya na za Hakimu Mkazi zitaendeshwa kwa Kiswahili ama Kiingereza, isipokuwa hukumu inaandikwa kwa Kiingereza.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mahakama Kuu, Kanuni za Lugha za Mahakana ukisoma Kanuni ya (2) inasema kuwa Lugha ya Mahakama Kuu itakuwa Kiswahili au Kiingereza, isipokuwa kumbukumbu za maamuzi, ama hukumu itakuwa kwa lugha ya Kiingereza.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni za Mahakama ya Rufani ya mwaka 2009, ukisoma Kanuni ya (5) lugha inayotumika katika kuendesha mashauri itakuwa ni Kiswahili au Kiingereza kulingana na maelekezo ya Jaji Mkuu au Jaji anayesikiliza shauri husika, isipokuwa hukumu inaandikwa kwa Kiingereza.
Mheshimiwa Spika, hivyo ninapenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba uendeshaji wa mashauri katika Mahakama zote nchini kwa mujibu wa Sheria na Kanuni zilizopo unaruhusu kutumia lugha zote mbili, Kiswahili na Kiingereza na tumekuwa tukizingatia lugha hizo katika uendeshaji wa mashauri.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:-
Kumekuwa na mgongano mkubwa wa Katiba kati ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba ya Zanzibar unaosababisha ongezeko la Kero za Muungano na mgongano wa kimamlaka baina ya Serikali mbili:-
Je, ni lini Serikali ya Muungano italeta mapendekezo ya mabadiliko ya Katiba ili kuondoa changamoto zilizomo ndani ya Katiba hizo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Kombo Hamad, Mbunge wa Wingwi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kikatiba hakuna mgongano mkubwa wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba ya Zanzibar unaosababisha ongezeko kubwa la Kero za Muungano wala mgongano wa kimamlaka baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka utaratibu mahsusi wa kushughulikia tafsiri ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano au utekelezaji wake inayobishaniwa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Hadi sasa hakuna upande wowote baina ya Serikali hizi mbili ambao una tafsiri tofauti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano au utekelezaji wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kuwa, hakuna mgongano wa Katiba kati ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba ya Zanzibar, Serikali haina sababu ya kuleta Mapendekezo ya Mabadiliko ya Katiba ili kuondoa changamoto hiyo ambayo haipo.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI (K.n.y. MARY P. CHATANDA) aliuliza:-
Mahakimu na Watumishi wa Mahakama hawajapandishwa vyeo kwa muda mrefu na hata wanaobahatika kupandishwa hawabadilishiwi mishahara:-
(a) Je, ni lini Serikali italifanyia kazi tatizo hilo?
(b) Kwa kuwa Wanasheria wengine hupewa house allowance: Je, kwa nini hawa nao wasipewe kama sehemu ya motisha lakini pia wapewe extra duty allowance?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mary Pius Chatanda, Mbunge wa Korogwe Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuwapandisha vyeo Watumishi wenye sifa stahiki ni wajibu endelevu wa Serikali. Mahakama ya Tanzania imekuwa ikichukua hatua kuwapandisha Mahakimu na Watumishi wa ngazi mbalimbali vyeo kuzingatia vigezo vilivyowekwa kisheria ikiwa ni pamoja na muda wa utumishi kazini, utendaji wa kazi, weledi na maadili pamoja na upatikanaji wa vibali kutoka Idara Kuu ya Utumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013, jumla ya Mahakimu na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji 52 walipandishwa vyeo. Mwaka 2013/2014, jumla ya Watumishi 200 walipandishwa vyeo, mwaka 2014/2015, jumla ya Mahakimu na Wasaidizi wa Sheria wa Majaji 22 na Watumishi 686 walipandishwa vyeo na mwaka 2015/2016, jumla ya Mahakimu na Wasaidizi wa Sheria 59 na Watumishi 447 walipandishwa vyeo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kutoa posho kwa watumishi wake kama sehemu ya motisha. Mahakama imeendelea kutoa motisha ya posho mbalimbali na stahili za watumishi kwa mujibu wa sheria, kulingana na uwepo au hali ya bajeti.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza:-
Wanawake wengi bado hawaelewi haki zao hasa kuhusu haki za kumiliki ardhi.
Je, kuna mkakati gani wa Serikali wa kuwawezesha wanawake waweze kujua haki zao za kumiliki ardhi?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi imekuwa ikitoa elimu kwa umma kuhusu haki ya wanawake kumiliki ardhi. Elimu hiyo imekuwa ikitolea kupitia njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na vipindi vya redio na luninga, mikutano ya hadhara, warsha, semina, maonesho mbalimbali kama vile Siku ya Sheria, Wiki ya Utumishi wa Umma, Siku ya Mtoto wa Afrika, Maadhimisho Siku ya Maadili na Haki za Binadamu, Wiki ya Msadaa wa Kisheria pamoja na maonyesho mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imekuwa ikichapisha machapisho yenye kuelimisha umma kuhusu masuala ya umiliki wa ardhi. Aidha, Tume hiyo imetoa elimu katika Kata 72 katika Wilaya 18 za Tanzania Bara na Shehia nane za Wilaya nne za Tanzania Zanzibar. Wilaya za Tanzania Bara ni Biharamulo, Ngara, Mpanda, Babati, Simanjiro, Mbarali, Mbeya, Mvomero, Ulanga, Ludewa, Makete, Nkasi, Namtumbo, Tunduru, Kahama, Kishapu, Kilindi na Tanga; na Wilaya za Tanzania Zanzibar ni Unguja Kusini, Unguja Kaskazini- A, Mkoani na Michweni.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kuendelea kuelimisha umma katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar hasa kwa wanawake ili wananchi wote waweze kufurahia haki zao za msingi ikiwemo haki ya kumiliki ardhi.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO aliuliza:-
Mahakama ya Wilaya ya Kasulu ni ya zamani sana, ni chakavu sana na wakati mwingine huduma hazitolewi kabisa.
• Je, ni kwa nini Serikali imeitelekeza Wilaya ya Kasulu?
• Je, mahakama hiyo itajengwa lini?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzungwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Kasulu ni chakavu. Hata hivyo, mpango wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/2017 ilikuwa ni kujenga upya jengo la Mahakama ya Wilaya ya Kasulu ambapo hadi sasa mkandarasi wa ujenzi huo ameshapatikana na anategemea kuingia makubaliano ya ujenzi huo mwishoni mwa mwezi huu wa Juni, 2017. Hivyo napenda kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 Mahakama itaanza utetelezaji wa ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Kasulu.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Katika Jimbo zima la Mlimba hakuna Mahakama hata moja, jambo linalosababisha mahabusu kupelekwa Jimbo la Kilombero umbali wa takriban kilometa 260 kuhudhuria mahakama:-
Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama katika Jimbo la Mlimba ili kuwaondolea wananchi adha ya kusafiri umbali mrefu katafuta huduma ya Mahakama?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Suzan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, uanzishaji wa Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo nchini unaongozwa na Sheria ya Mahakimu, Sura 11 ya Sheria za Tanzania (The Magistrate Courts Act, Cap. 11) of the laws of Tanzania. Kifungu cha 3(1) kinaeleza kuwa katika kila Wilaya kutaanzishwa Mahakama za Mwanzo; Kifungu cha 4(1) kinaeleza kuwa kutaanzishwa Mahakama za Wilaya katika kila Wilaya na Kifungu cha 5(1) kinampa mamlaka Jaji Mkuu kutoa amri ya kuanzisha Mahakama za Hakimu Mkazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Mlimba, Tarafa ya Mlimba ipo Mahakama ya Mwanzo inayoendelea kutoa huduma hadi hivi sasa. Serikali inatambua kuwa miundombinu ya Mahakama hiyo hairidhishi na hivyo katika mwaka wa fedha 2017/2018 tumepanga kujenga Mahakama ya Mwanzo mpya katika Tarafa ya Mlimba.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umbali na ukubwa wa Wilaya ya Kilombero yenye Majimbo ya Kilombero na Mlimba na itajitahidi kuhakikisha kwa kadri ya uwezo utakavyokuwa kujenga Mahakama za Mwanzo za kutosha katika Wilaya nzima ya Kilombero ili kusogeza huduma za Mahakama na utoaji haki karibu zaidi na wananchi.
MHE. JOSEPH R. SELASINI aliuliza:-
Wapo wananchi wengi waliotuhumiwa na kushtakiwa katika Mahakama tofauti na kutozwa faini na baada ya kulipa faini hizo wakakata rufaa Mahakama za juu kulalamikia hukumu hizo na Mahakama za juu zikawaona hawana hatia.
(a) Je, Serikali inayo kumbukumbu ya taarifa za wananchi wa namna hiyo?
(b) Na kama Serikali inazo taarifa hizo, je, ni lini wananchi hao watarejeshewa fedha zao?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Roman Selasini, Mbunge wa Rombo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inazo kumbukumbu zote na taarifa za wananchi wanaolipa faini na baadae kushinda rufaa za kesi zao na hivyo kustahili kurejeshewa faini walizotoa kwani mashauri yote na hukumu zinazotolewa kumbukumbu zake zinatunzwa na Mahakama. Urejeshaji wa fedha hutegemea upatikanaji wa nyaraka zinazothibitisha malipo ya faini kupokeleawa na uwepo wa nakala ya hukumu kwani mara nyingi rufaa inaweza kuwa imetolewa baada ya muda mrefu tangu hukumu ya kwanza kutolewa.
Mheshimiwa Spika, utaratibu unaotumiwa na Mahakama ni kuwasilisha hazina nyaraka husika kwa ajili ya uhakiki na uidhinishwaji wa malipo kabla ya fedha zao kurejeshwa tena Mahakamani ili mwananchi husika aweze kulipwa. Kwa mwaka wa fedha 2015/2016 na mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi 60,152,487.65 zililipwa na Mahakama kama fidia kwa mashauri 16 yaliyohakikiwa na kuthibitishwa na Mahakama baada ya kupokea fedha kutoka Hazina.
Mheshimiwa Spika, madai 24 yenye jumla ya shilingi 87,046,649.38 yameshachambuliwa na kuwasilishwa Hazina na tayari yanasubiri malipo na wakati huo huo jumla ya madai 12 yenye thamani ya shilingi 6,920,000 miongoni mwao yakiwemo madai mapya yamewasilishwa Hazina. Mara uhakiki utakapotengamaa na Mahakama kupokea fedha kutoka Hazina malipo hayo yatafanyika bila kuchelewa.
Mheshimiwa Spika, kama kuna mtu yeyote ambaye amecheleweshewa malipo yake nashauri awasiliane na Wizara au Mahakama ili kutatua tatizo hilo.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-
Mkoa wa Simiyu hauna Mahakama ya Mkoa licha ya Mkoa huo kuanzishwa zaidi ya miaka mitano iliyopita. Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya ngazi ya Mkoa?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi katika mikoa yote Tanzania Bara. Mkoa wa Simiyu kama ilivyo mikoa mingine unayo Mahakama ya Hakimu Mkazi ambayo kwa sasa inatumia jengo la kupangisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ya Serikali ni kuwa na jengo la Mahakama kwa kila ngazi kwa kadiri itakavyowezekana. Tayari tunao mpango wa kujenga majengo katika kila ngazi ya Mahakama kwa awamu katika mwaka wa fedha 2017/2018. Simiyu ni moja ya mikoa mitano ambayo ujenzi wake wa Mahakama umeanza ambapo kwa sasa msingi umekamilika na hatua nyingine za ujenzi zinaendelea.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Chuo cha Mahakama Lushoto (IJA) kinatoa taaluma ya Stashahada za Sheria.
(a) Je, ni lini sasa Serikali itaongeza uwezo wa Chuo hicho ili kitoe elimu ya sheria kwa ngazi ya Shahada?
(b) Je, ni kwa nini Serikali sasa isione umuhimu wa kukifanya Chuo hicho kiwe Wakala wa Law School ili mafunzo ya uwakili pia yaweze kutolewa chuoni hapo?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, madhumuni ya kuwepo kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kutoa elimu endelevu kwa watumishi wa Mahakama na watumishi wa sekta nyingine za umma wakitokea kazini na siyo kutoa elimu ya sheria kwa ngazi ya shahada. Nia na makusudi hayo inalenga katika kuwaimarisha watumishi hao wanapokuwa kazini kwa kuwapatia mbinu na nyenzo muhimu ambazo ni nadra kupatikana wakati wanapokuwa shuleni/vyuoni na hivyo kuwasaidia katika kutekeleza majukumu yao ya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara bado tunaona kuwa kuna umuhimu wa kuendelea kusimamia lengo la kuanzishwa kwa chuo hicho kwani bado ni la msingi katika kuimarisha kitaaluma watumishi wa Mahakama na sekta nyingine nchini. Hata hivyo, kimeunda kikosi kazi cha kutafiti maeneo mapya ya uanzishwaji wa kozi mpya ikiwemo mafunzo ya ngazi ya Shahada ya Sheria katika Uongozi wa Mahakama (Bachelor of Law in Judicial Administration).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema, msingi wa kuanzishwa kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni kutoa elimu kwa wanaotokea kazini ili kuwapatia nyenzo muhimu kuweza kutekeleza majukumu yao vema. Mafunzo yatolewayo na Chuo cha Uanasheria kwa vitendo yanalenga kumuandaa mhitimu wa shahada ya kwanza kutekeleza kazi ya Uwakili ya Uanasheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Chuo cha Lushoto lengo ni kumwongezea mbinu za kutekeleza kazi za kutoa haki yaani Mahakimu na Majaji, mafunzo ambayo yanatolewa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nachukua ushauri wa Mheshimiwa Mbunge ili kuangalia namna njema ya kuoanisha mafunzo yanayotolewa na vyuo hivi viwili.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-
Je, Idara ya Mahakama iliandika Ripoti za Sheria (Law Reports) ngapi kwa mwaka 2017?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, Tanzania inatumia mfumo wa kisheria wa Common Law ambao maamuzi ya Mahakama za juu yana nguvu ya kisheria na yanazibana Mahakama nyingine za chini katika kufanya maamuzi ya kesi. Msingi huo wa kisheria unaofahamika stare decisis unazitaka Mahakama kutumia misingi ya tafsiri ya kisheria yaliyotolewa na Mahakama za juu na wakati mwingine zilizoamuliwa na Mahakama iliyo na mamlaka sawa endapo kesi zinafanana. Hata hivyo, Mahakama ya juu kabisa kama ilivyo Mahakama ya Rufani hapa Tanzania inaweza na ina mamlaka ya kubadilisha msingi au tafsiri ya sheria iliyotajwa huko nyuma inaposikiliza shauri jipya.
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha msingi huo unafuatwa, uchapishaji wa mara kwa mara wa maamuzi ya Mahakama katika Law Reports ni muhimu ili wanasheria, Majaji na watu wote waweze kujua ni msingi gani na uamuzi upi wa sheria umewekwa na Mahakama katika kesi fulani iliyofikishwa Mahakamani na kuamuliwa. Kwa kufuata utaratibu huo, tangu mwaka 1921 Law Reports zimekuwa zikichapishwa Tanzania. Hivyo basi, taarifa za sheria ni mfululizo wa vitabu ambavyo vina maoni ya Mahakama kutoka kwenye baadhi ya kesi zilizoamuliwa na Mahakama ambazo zinatakiwa kufuatwa na Mahakama nyingine.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2017 Mahakama ya Tanzania kupitia Bodi ya Uhariri ya Taarifa za Sheria za Tanzania (Tanzania Law Reports Editorial Board) imeandaa Law Reports zipatazo nne ambazo ni Law Report ya mwaka 2014, 2015, 2016 na 2017. Kwa sasa Law Reports hizo zipo katika hatua na taratibu za mwisho ikiwa ni pamoja na kufanyiwa uhakiki wa kina wa kiuhariri na taratibu zingine za ununuzi kwa ajili ya kumpata mzabuni wa kuchapisha Law Reports rasmi.
MHE. BONIPHACE M. GETERE (K.n.y. LAMECK O. AIRO) aliuliza:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Rorya ilianzishwa mwaka 2007 na ina ukubwa wa kilometa za mraba 9,345 na idadi ya watu wapatao 400,000, lakini inakabiliwa na tatizo la uhaba wa watumishi katika Mahakama za Mwanzo za Kineri, Ryagoro, Obilinju na Shirati; hadi sasa Wilaya ya Rorya inatumia Mahakama ya Wilaya ya Tarime hali inayosababisha kesi kuchelewa kusikilizwa kwa wakati:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Mahakama ya Wilaya kwenye Jimbo la Rorya?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lameck Okambo Airo, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango wa Mahakama wa kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama katika ngazi mbalimbali, Mahakama ya Wilaya ya Rorya imepangiwa kujengwa katika Mwaka wa Fedha 2019/2020.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI aliuliza:-
Katika Kata ya Magoma, Korogwe Vijijini kumejengwa Mahakama ya Mwanzo ya Kisasa, lakini toka ijengwe imefika miaka saba sasa haijafunguliwa:-
Je, ni lini Serikali itafungua Mahakama hiyo ili wananchi waachane na usumbufu wa kufuata huduma za Mahakama Korogwe?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stephen Hillary Ngonyani, Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mahakama ya Mwanzo ya Magoma ilijengwa muda mrefu kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge wa Korogwe, lakini jengo lile halikukamilika. Mahakama iliyojengwa ni ya kisasa, iliyohusisha ujenzi wa jengo la Mahakama, nyumba ya Hakimu na kantini.
Mheshimiwa Naibu Spika, majengo haya yalisimama kwa muda mrefu kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa fedha. Mradi huu sasa umefufuliwa na unatekelezwa na SUMA JKT, chini ya usimamizi wa TBA Mkoa wa Tanga na unatarajiwa kukamilika na kuanza kutumika kabla ya Julai mwaka huu 2018.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-

Wakazi wa Jimbo la Mkalama wanapata shida sana kufuata huduma za Mahakama katika Wilaya ya Iramba – Kiomboi, umbali mrefu kutoka Mkalama:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Wilaya yalipo Makao Makuu ya Wilaya ya Mkalama?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuanzisha Mahakama ya muda ya Wilaya katika majengo ya Mahakama ya Mwanzo Nduguti?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Iramba Mashariki, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama imejiwekea mkakati wa kujenga na kukarabati majengo ya Mahakama kwa awamu, lengo likiwa ni kuwa na majengo katika wilaya zote ifikapo mwaka 2021. Katika mkakati huo, jengo la Mahakama ya Wilaya ya Mkalama limepangwa kujengwa mwaka 2019 na 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge kuhusu kutumia jengo la Mahakama ya Mwanzo Nduguti kuanzisha huduma za Mahakama ya Wilaya. Hata hivyo, tumefanya tathmini na kubaini kuwa jengo linalotumika sasa kwa Mahakama ya Mwanzo ya Nduguti halitoshelezi kuendesha Mahakama ya Wilaya na ya Mwanzo kwa kuwa mahitaji ya huduma za Mahakama za Mwanzo bado ni makubwa. Mpango tulionao ni kuanzisha Mahakama ya Wilaya katika Mahakama ya Mwanzo Iguguno, ujenzi wa jengo jipya katika Mahakama ya Mwanzo Iguguno umekamilika na kwa tathmini iliyofanyika linaweza kutumika kwa Mahakama ya Wilaya ya Mkalama na Mahakama ya Mwanzo Iguguno kwa muda wakati mipango ya kujenga ya ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tunaendelea kukamilisha taratibu za upatikanaji wa vifaa, watumishi, pamoja na taratibu za kisheria ili kuweza kuanzisha Mahakama hiyo kabla ya mwisho wa mwezi Juni, 2019.
MHE. FATMA H. TOUFIQ aliuliza:-

Miongoni mwa sababu kubwa zinazosababisha wanawake na watoto kuporwa mali zao na ndugu za waume zao ni kukosekana kwa wosia, jambo ambalo jamii haijaona umuhimu huo wakiamini kuwa kuandika wosia ni kujitakia kifo:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani endelevu wa kukabiliana na kadhia hii?

(b) Je, Serikali itakuwa tayari kuielimisha jamii umuhimu wa kuandika wosia kama njia mojawapo ya kulikabili tatizo hili ambalo ni kubwa katika jamii?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuandika wosia kama njia mojawapo ya kukabiliana na migogoro katika jamii inayohusiana na mgao wa mali za marehemu. Kwa kutambua hilo, mwaka 2008, Wizara yangu kupitia Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi (RITA) iilianzisha huduma ya kuandika na kuhifadhi wosia ikiwa ni pamoja na kuuelimisha umma kuhusiana na huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu wakati huo, Wizara yangu kupitia Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi inaendelea kubuni na kutekeleza mikataba ya aina mbalimbali ili kuhakikisha na kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuandika na kuhifadhi wosia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukitumia njia mbalimbali kutoa elimu ya kuandika wosia ikiwa ni pamoja na mikutano ya hadhara, redio, televisheni, vipeperushi, magazeti na mitandao ya kijamii. Pamoja na jitihada hiyo, mpaka sasa tumeweza kuandika na kuhifadhi wosia 578 kati ya hizo 32 tayari zimeshatumika. Hata hivyo, idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na idadi kubwa ya Watanzania waliopo kwa sasa. Bado kuna changamoto ya uelewa kwa wananchi wengi juu ya umuhimu wa suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kulithibitishia Bunge lako Tukufu kuwa Wizara yangu itaendelea kubuni njia mbalimbali za kuelimisha jamii kuwa umuhimu wa kuandika wosia ikiwa ni jitihada mojawapo ya kukabiliana na migogoro ya mgao wa mali za marehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba kutumia fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote kuchangia katika juhudi zinazofanywa na Serikali za kuhamasisha wananchi kujijengea tabia na utamaduni wa kuandika na kuhifadhi wosia sehemu maalum hadi utakapohitajika. Endapo wananchi watahamasika, tutakuwa tumeondokana na migogoro isiyo ya lazima na hivyo kuruhusu maendeleo ya ustawi wa jamii. Hii ni njia muhimu ya kulinda haki za wanawake na watoto waliofiwa ndani ya familia.
MHE. OTHMAN OMAR HAJI aliuliza:-

Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu (ACPHR) inatumia jengo la TANAPA lililopo Arusha kwa mkataba wa upangaji baina ya TANAPA na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ulioanza tarehe 1 Desemba, 2008 kwa kodi ya dola za Marekani 38,998.89 kwa mwezi:-

Je, kati ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu ni nani mwenye jukumu la haki za binadamu na nani mwenye jukumu la kulipa kodi ya jengo hilo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Othman Omar Haji, Mbunge wa Gando, kama yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo mwaka 2007, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Umoja wa Afrika Mashariki ziliingia Mkataba wa Uenyeji (Host Agreement) wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Katika mkataba huo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano ndiyo msimamizi na mtekelezaji mkuu wa mkataba huo kwa niaba ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 5(1) ya mkataba kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Umoja wa Afrika Kuhusu Uenyeji wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, inaeleza kuwa Tanzania kwa gharama zake inawajibika kutoa majengo kwa ajili ya ofisi ya mahakama na makazi ya Rais na Msajili wa Mahakama hiyo. Aidha, Ibara ya 5(2) inaipa Tanzania jukumu la kutoa ofisi ya muda kwa ajili ya mahakama husika wakati ikiendelea na taratibu za kupata jengo la kudumu la mahakama. Kutokana na kipengele hicho Serikali iliingia mkataba na TANAPA wa kukodisha majengo yale ili kuwa ofisi ya muda ya Mahakama ya Haki za Binadamu na Watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maelezo hayo, ni dhahiri kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ndiyo yenye jukumu la kulipa kodi hiyo kutokana na makubaliano yaliyofikiwa. Hata hivyo, suala la kulinda haki za binadamu ni suala la kila mtu na kila taasisi sehemu yoyote duniani. Kimsingi, hata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inahusika moja kwa moja katika kulinda haki za binadamu.
MHE. MGENI JADI KADIKA aliuliza:-

Katika jitihada za nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki za kuboresha uchumi, viongozi wa Jumuiya hiyo walipitisha utengenezaji wa Bandari ya Wete – Pemba;

Je, mpango huo umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA
MASHARIKI) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum napenda kutoa maelezo mafupi kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Bandari ya Wete ni mojawapo ya miradi 17 ya mfano (flagship projects) inayosimamiwa na wakuu wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyopitiswa katika mkutano wao wa kazi (retreat) uliofanyika mwezi Februari, 2018 Jijini Kampala, Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi inayotekelezwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki ni ile yenye sura ya kikanda (Mradi uweze kunufaisha nchi zaidi ya moja) ambapo nchi wanachama wamekubaliana kuitekeleza kupitia utaratibu wa kutafutiwa fedha kutoka kwa wabia wa maendeleo na kuitangaza kwa wawekezaji kikanda. Miradi hiyo hutekelezwa kwa kuzingatia mikataba inayoingiwa na nchi wanachama inayowezesha kukopeshwa fedha za utekelezaji. Aidha, ulipaji na gharama za utekelezaji wa miradi hiyo hufanywa na nchi mwanachama inayonufaika moja kwa moja kutokana na mradi husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kuendeleza mradi wa Bandari ya Wete upo palepale Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuendelea kuifanyia matengenezo bandari hiii ili iendelee kutoa huduma nzuri kwa wananchi. Matengenezo ambayo yamekwishafanyika ni pamoja na kutengeneza upana wa gati kufikia mita tisa na urefu wa mita tatu kuelekea baharini, na kulikarabati gati yote yenye urefu wa mita 54. Matengenezo hayo yaligharimu kiasi cha shilingi 473.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar imeshafanya mazungumzo na mwekezaji mzawa katika kuendeleza Bandari ya Wete. Tayari makubaliano ya mwanzo baina ya Wizara husika kupitia Shirika la Bandari Zanzibar na mwekezaji yameshafanyika na hivi sasa mwekezaji kwa kushirikiana na wataalam wa shirika la bandari wamo katika maandalizi ya kufanya upimaji (surveying) ya eneo lililopendekezwa kuwepo bandari ili kutayarisha michoro (usanifu) inayohitajika kuwezesha hatua nyingine za ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuhakikisha miradi ya kipaumbele iliyopitishwa na wakuu wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki yenye maslahi mapana kwa Taifa letu inatekelezwa ikiwa ni pamoja na kufuatilia upatikanaji wa rasilimali fedha.