Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Anne Kilango Malecela (29 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza leo kwa sababu ni mara ya kwanza kuongea katika Bunge hili la Kumi na Moja, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mtoa haki. Pili, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniona, kwa kutambua mchango wangu na kunirejesha Bungeni. Namshukuru sana, namshukuru sana, namshukuru sana! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu nitachangia kitu kimoja tu. Nitachangia ukurasa wa 21 Kifungu cha 31 kuhusu kilimo. Hotuba yangu itakuwa ni ndefu, kwa hiyo, nusu nitaongea kwenye hotuba ya Waziri Mkuu sitamaliza, nusu nitaongea kwenye Wizara ya Kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wizara ya Kilimo na nitaongea kitu kimoja kuhusu tangawizi. Leo naiongea tangawizi kwa mapana yake. Watu wanaweza wakajiuliza, hii tangawizi ni nini? Wengine hawaelewi tangawizi ni nini. Tangawizi ni zao la viungo (Spices), lakini tangawizi ni
malighafi ya kutengeneza dawa za binadamu, kutengeneza cosmetics, nikiwa na maana ya vipodozi, vinywaji na vitu vingine vidogo vidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niigawe hii tangawizi katika mafungu matatu; kwanza nitaiongea tangawizi kiulimwengu, kwa Afrika na mwisho nitaiongea kwa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, duniani hapa, ulimwenguni, nchi bora tano zinazoongoza kwa kulima tangawizi ya kwanza ni India, lakini India inaongoza kwa kulima tangawizi duniani na inayoongoza kwa kutumia tangawizi duniani. Nchi ya pili ni China; ya tatu ni Nepal; na ya nne ni Nigeria. Ni nchi ya Kiafrika hii na inalima tangawizi kweli na ina-export tangawizi kwa wingi mno.
Waheshimiwa Wabunge, kama mnasoma vitabu vya kilimo, utakuta kwamba Nigeria imekuwa inategemea zao la tangawizi kwa export mpaka ilipofika mwaka 1960 ndipo ilipogundua mafuta, ikawa mafuta yako juu kwa tangawizi. Sisi huku, nikisema tangawizi, watu wanasema, “huyu naye na tangawizi!” Tangawizi ni zao zuri sana na lina export nzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi ya nne ni Nigeria kwa hiyo ni ya kwanza kwa Afrika. Nchi ya tano ni Thailand. Nisiishie hapo kwa upande wa ulimwengu, twendeni tuangalie nchi zinazo- export tangawizi kwa wingi. Sasa kwa sababu India inalima tangawizi kwa wingi, lakini anaiconsume yeye mwenyewe sana. Ameshindwa kuwa wa kwanza kwenye ku-export. Nchi ya kwanza inayo-export tangawizi kwa wingi ni China; ya pili inakuja kuwa India; ya tatu, watu hawataamini, Nigeria ni giant number three kwa ku-export tangawizi; ya nne inakuwa ni German na Netherland.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nirudi Afrika. Nilitaka kutoa picha ya tangawizi na ulimwengu kidogo tu. Twende Afrika sasa. Nigeria inaongoza kwa kulima tangawizi Afrika. Nigeria inajipambanua kwamba kwa nini inaongoza kulima tangawizi na ku-export? Inasema kwa nini inafanya hivyo? Kwa nini imeweza? Inasema ina ardhi kubwa sana yenye rutuba; inasema, ina mvua za kutosha na mito isiyokauka, lakini inasema ina hali ya hewa nzuri, ndiyo maana imeweza kuwa na comperative advantage upande wa tangawizi kuliko nchi zote za Afrika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Nigeria imefika hapo, kwamba ina-export tangawizi inapeleka USA, Europe, Morocco na nchi nyingi tu. Kitu cha ajabu, yenyewe kama Taifa inakubali kwamba wakulima wakubwa wa tangawizi kwa Nigeria asilimia 40 ni wanawake. Wanawake wa Nigeria ndio walioshika mashamba makubwa ya tangawizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hali ya hewa ya Nigeria, nakubali ni nzuri; ardhi ya Nigeria, nakubali ni nzuri. Ile hali ya hewa ya Nigeria ambayo imeruhusu kulima tangawizi, ipo Tanzania! Ukisema mvua, Tanzania tuna mvua; ukizungumza mito isiyokauka; tunayo, twende tuone mfano. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Mkoa wa Ruvuma kuna mvua ya kutosha; Mkoa wa Njombe una mvua ya kutosha; Mbeya ina mvua ya kutosha, Rukwa na kigoma; Tanzania haina maana kwamba hatuna sehemu zenye hali ya hewa nzuri, haina maana kwamba hatuna mito ya
kutosha, haina maana kwamba hatuna ardhi ya kutosha. Kwa nini wenzetu wamefanikiwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Nigeria imethamini zao la tangawizi, imekwenda imesimama imara kwenye zao la Tangawizi, lakini kwetu sisi, Kipare tuna methali inasema, “Ng’ombe kuramoshe ukuhundue.” Ina maana Ng’ombe anajipeleka mwenyewe machungani, anajirudisha
mwenyewe. Wakulima wa Tanzania wanaolima tangawizi wako wenyewe. Serikali haijasimama imara ikalishika hili zao, ikatayarisha project maalum ya ku-study hili zao la tangawizi na ikasimama imara ikatafuta hili zao wapi tutalilima? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuwa na Tanzania ya viwanda kama hatutakuwa na kilimo bora, hatuwezi. Itakuwa tunasema, Tanzania ya viwanda, Tanzania ya viwanda! Ni lazima tukaboreshe kwanza kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hili nitaliongea miaka mitatu na nusu. Naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge, Jimbo langu sasa ni Tangawizi. Nitazunguka nchi nzima kuhakikisha naboresha kilimo cha Tanzania na nina uhakika Serikali mtaniunga mkono kila siku. Ofisi nitakayokwenda
kuiona mimi ni Ofisi ya Wizara ya Kilimo. Nitakwenda, nitashauri, nitapita, nitakwenda, nitarudi. Serikali naomba zao la tangawizi hebu tuliangalie, tukae, tuandike project, tutafute wenzetu wa Nigeria, twende tukai-visit Nigeria; siyo lazima mtulipie nauli, tutalipa wenyewe. Mimi nitakwenda Kaduna nikajue kwa nini Kaduna wanalima tangawizi kwa wingi? Nitafanya hiyo kazi. Hatuwezi kuzungumza suala la viwanda kwa nguvu, tutafika, lazima tujenge viwanda; kilimo kiko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumze ukweli; zao la tangawizi ndugu zangu, ukiona Muhindi, ni very aggressive huku duniani; Mchina ni very aggressive; MNigeria ni very aggressive; kwa nini haya Mataifa matatu yanasimama kulima tangawizi? Wanajua faida yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo, naomba niishie nusu ya hotuba yangu. Wizara ya Kilimo, naendelea na zao la tangawizi na nitachangia kwa maandishi, nitamletea Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kabla sijamaliza, nirudi niseme naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Nilikuwa nje kwa mwaka mmoja na miezi kadhaa. Nilikuwa nawaangalia mnavyochacharika, Serikali mnafanya kazi sana, lakini naomba mwongeze nguvu kwenye kilimo cha Tanzania. Ni lazima tuondoke hapa tulipo. Tutaondoka tu kama tutakuwa na viwanda vya uhakika. Hilo linawezekana iwapo tutashirikiana wote tena tukitaka kujenga nchi vizuri, tushirikiane bila kujali itikadi zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE.ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge, hizi Wizara mbili ni muhimu sana hebu kila mtu atumie dakika kumi vizuri zaidi kuliko kuzipoteza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niseme mimi nimekuwepo Bungeni hapa tangu mwaka 2000. Suala nitakaloliongea leo nimeliongea tangu mwaka 2001, naongelea upande wa TAMISEMI. Wilaya ya Same ni kubwa sana katika Mkoa wa Kilimanjaro. Mkoa wa Kilimanjaro una
Wilaya saba lakini Wilaya ya Same ina ukubwa wa kilomita za mraba 5,152 ambazo ni sawa na asilimia 40 ya Mkoa mzima wa Kilimanjaro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Same hiyo ina majimbo mawili, Same Magharibi na Same Mashariki. Makao Makuu ya Wilaya yako Same Magharibi yako katika Kata ya Same ambayo ndiyo ya mwisho unakwenda Wilaya ya Mwanga. Jimbo la Same Mashariki liko mwishoni na Mkoa wa Tanga. Kata ya kwanza inaanza Bendera, Kiurio, Ndungu, Kalemawe, Maore hapa ni tambarare.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo linapojitokeza ni hapa. Tunapata tatizo kwamba Hospitali ya Wilaya ya Same iko, Kata ya Same ambako ni mbali sana na Jimbo la Same Mashariki. Kwa hiyo, athari kubwa inawakuta kina mama wajawazito, hili suala nimeliongelea kwa miaka 15. Kina mama wengi sana kutoka Jimbo la Same Mashariki wanapohitaji huduma ya upasuaji dakika za mwisho anataka kujifungua anagunduliwa kwamba upasuaji unahitajika ni lazima apelekwe Same, wengi sana wanapoteza maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia 2010-2015 tumepoteza akina mama 18 na watoto wao. Hao ni wale waliofika Same. Waliopotezea maisha majumbani au kwenye zahanati sina takwimu za kusema.Watoto wachanga 28 wamepoteza maisha. Namshukuru sana Mheshimiwa Jafo alikuja Wilaya ya Same. Wabunge hatukuwa na habari tungekuja tukulalamikie kule kule, lakini mimi kwa sababu nimesema kwa miaka 15 naiomba sasa TAMISEMI ione umuhimu wa hapa Ndungu ndani ya Jimbo la Same Mashariki kwenye Makao Makuu ya Jimbo la Same Mashariki, kile kituo cha afya kipate huduma ya upasuaji. Inapokuja kuzungumzia akina mama nitapaza sauti mpaka dakika ya mwisho. Jimbo la Same Mashariki akina mama wanapoteza maisha sana kwa sababu ya kukosa huduma ya upasuaji. Kipare tunasema; “wekienda kutana na nashindaki taganyamaa.” Naomba nitafsiri, wewe kama umebeba nyama kichwani nzi watakufuata. Sasa kama unataka wale nzi wasikufuate hiyo nyama itupe. Hili suala ili nisilipigie makelele Serikali malizeni hili jambo, hamtanisikia tena nikisema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapo nimetoka TAMISEMI nije Wizara ya Utumishi na Utawala Bora. Mimi nazungumzia Mfuko wa Rais wa Kujitegemea. Huu Mfuko wa Rais wa Kujitegemea umeanza takribani miaka 33 iliyopita.
Mimi nimeungalia vizuri Waheshimiwa Wabunge, huu mfuko unawasaidia akina mama na vijana wanapata mahali pa kukopea kwa ajali ya miradi midogo dogo ya kujiendeleza ili waweze kujitengemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huku duniani, nizungumzie Tanzania na Afrika akina mama pamoja na vijana ni wazalishaji wakubwa sana na mjue akina mama ndiyo wanaoangalia vijana, sijui mmenielewa? Kwa hiyo, mama anacheza kotekote anazalisha na anaangalia vijana. Huu
Mfuko wa Rais wa Kujitegemea takribani miaka 33 sasa hivi lakini umeonyesha kufanya vizuri sana. Kwa sababu gani nasema hivyo Mwenyekiti? Inapokuja kwenye marejesho hawa wanarejesha asilimia mia moja hakuna matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naomba nizungumze kwa unyenyekevu. Kwanza tuwapongeze wanaoratibu mfuko huu kwa sababu mahali popote ambapo kuna kukopa kurejesha kuna matatizo, lakini hawa wanarejesha asilimia 100 ina maana wanaoratibu mfuko huu
wanafanya kazi vizuri sana. Hata hivyo, kuna changamoto kwamba Serikali haiwapi pesa za kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo huu Mfuko wa Rais wa Kujitegemea inapokuja kwenye repayment ni 100% jamani kwa nini wasipewe fedha za kutosha? Kazi wanayoifanya inawasaidia akina mama na vijana kwa hiyo moja kwa moja inachangia kwenye uchumi. Naiomba Serikali
mfuko huu uangaliwe vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hapo tu, tangu 33 iliyopita mfuko huu uko kwenye Mikoa mitano tu ya Dar es Salaam, Lindi, Njombe na mwingine wa tano mniwie radhi nimeusahau.
Ombi langu kwa unyenyekevu mkubwa, Mheshimiwa Waziri wa Utumishi naomba unisikilize, kwa sababu marejesho ni 100% hebu sasa ongezeni mikoa mingine mitano. Katika hiyo mikoa mitano itakayoongezwa naomba Mkoa wa Kilimanjaro uwepo. Ukienda Same Magharibi akina mama wa Ruvu wanalima vitunguu wakipata mikopo watafanya kazi vizuri. Ukija Same Mashariki kuna akina mama wanaolima tangawizi na mpunga wakipata mikopo hiyo watafanya kazi vizuri zaidi. Naomba iongezwe mikoa mingine mitano na huu mfuko upewe pesa za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kupata nafasi, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba yangu nilianzia kwnye bajeti ya Waziri Mkuu nikatoa 50 percent, nikazungumzia suala la tangawizi ka ulimwengu, nikazungumzia suala la tangawizi kwa Afrika na nikasema nusu nitazungumzia suala la tangawizi kwa Tanzania na ninaanza hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakapozungumzia tangawizi Tanzania moja kwa moja utaigusa Wilaya ya Same, upande wa Mashariki mwa Wilaya ya Same ambao wao wenyewe katika nchi hii wanalima takribani asilimia 60.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna asilimia 40 iliyobaki, asilimia 40 sasa hivi inalimwa na Songea Vijijini ukienda Jimbo la Madaba wanalima tangawizi sana, ukienda Mkoa wa Kigoma wameanza kulima tangawizi sana kwa hiyo, ukiangalia vizuri Tanzania sasa hivi zao la tangawizi linakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuzungumzie safari ya maendeleo. Maendeleo ni safari ambayo ina misuko suko sana, hasa niongelee maendeleo yanayotupeleka kwenye viwanda na uchumi wa kati. Tusitegemee tufike kwenye viwanda, tufike kwenye uchumi wa kati kwa lele mama ni lazima tukutane na misukosuko mingi. Sasa mimi naomba niizungumzie hii hii tangawizi ya Same Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilianza kuwa Mbunge mwaka 2005 Same Mashariki, niliwakuta wananchi wanalima tangawizi. Mwaka 2007 mimi ndiyo nikaasisi wazo la kujenga Kiwanda cha Kusindika Tangawizi pale Same Masharuki. Tulianza kwa misukosuko mingi, lakini nakumbuka mwaka 2008 Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyepita Mheshimiwa Mizengo Pinda alikuja akaweka jiwe la msingi, tukajenga, tukahangaika mimi na Halmashauri na wananchi wakati huo tulikuwa na wana ushirika 613, wao walichangia shilingi 6,000, mimi kama Mbunge pamoja na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne tulifanya fund raising tukapata shilingi milioni 301; Halmashauri ikachangia shilingi milioni 45, lakini na Serikali ikatujengea godown lenye thamani ya milioni 287 na safari ikafikia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nizungumze kitu ambacho kinanipa nguvu sana leo na ninaomba Waheshimiwa Wabunge mfurahi pamoja na mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais amekuja na kauli ya Tanzania ya viwanda, lakini Mheshimiwa Rais kazi anayofanya ni kuchochea na kuwavuta watu, kuivuta mifuko ya jamii iwekeze kwenye viwanda kwa sababu by principle Serikali haijengi viwanda, lakini ina-facilitate. Sasa nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na nashukuru kwamba yupo hapa. Leo nazungumza jambo ambalo limenifariji sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani zangu za pili, tena hizi ni shukrani za unyenyekevu na moyo uliopondeka sana nipeleke kwa Bodi ya Wadhamini wa LAPF, nipeleke shukurani zangu za dhati kwa Mkurugenzi Mkuu wa LAPF Ndugu Eliud Sanga kwa sababu LAPF imekubali kuingia ubia na kile kiwanda nilichokijenga miaka ile. Leo tunazungumza LAPF inakwenda Same Mashariki, inakwenda Miamba, inakwenda kuingiza zaidi ya shilingi bilioni moja kwenye kile kiwanda, sasa hapo unazungumzia ile ndoto niliyokuwa naiona kila siku. Nilikuwa natamani tupate kiwanda kama cha Kaduna, Nigeria kwasababu gani sasa mimi nimepata furaha? LAPF inadhania imefanya kitu kidogo, hapana, imefanya mambo matatu makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, LAPF kwa kuingia ubia na Kiwanda kile cha Same Mashariki cha Tangawizi cha Miamba inepanua kilimo cha tangawizi Tanzania kwa sababu wakulima wa tangawizi wa nchi nzima watakuwa na uhakika wa kupata soko. Kiwanda kile kinajengwa na watu wenye uwezo wa kifedha, kinapanuliwa lakini walima tangawizi wote wa nchi hii, walima tangawizi wa Madaba, Wilaya ya Same, Kigoma wote watakuwa wana mahali pa kuuza tangawizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, inatuweka kwenye nafasi nzuri ya sisi kuingia kwenye export. Nigeria wenyewe kupitia kiwanda chao cha Kaduna kinachoitwa Kachia wana-export asilimia tisa yaani katika soko la dunia ile tangawizi iliyoko kwenye soko la dunia kuna asilimia tisa kutoka Kaduna. Hii ni kwa sababu wana Kiwanda kikubwa cha Tangawizi cha Kachia ambacho kiko kwenye state ya Kaduna ambapo wananchi wa Nigeria wanaolima tangawizi wote wanauzia pale na kile kiwanda kina-export 92 percent ya tangawizi ambayo inasindikwa pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi ninakiona Kiwanda cha Miamba, hiki ambacho LAPF sasa inaingia ubia pale kama ni pacha wa hiki Kiwanda cha Kaduna cha Nigeria. Hivyo hapo lazima tukubali kwamba LAPF imemuunga mkono Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais anazungumzia viwanda kwenye nchi hii, anachochea viwanda kwenye nchi hii, LAPF ilipokwenda kuingia ubia na kile kiwanda cha tangawizi imemuunga mkono Mheshimiwa Rais, ninawashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la tatu ambalo si dogo; hakuna kitu kinachomuumiza mkulima kama alime halafu hana soko. Mimi ninalima tangawizi si kwamba ninaihubiri tu, mimi ni muanzilishi wa kile kiwanda, nalima tangawizi. Kule Same nimekosa nafasi kwa sababu ardhi ya Same yote imejaa tangawizi kwa hiyo imebidi nitafute makazi, mimi nina makazi yangu Madaba kwa Mheshimiwa Mhagama, nalima tangawizi, nimeanza na hekari 20, kuanzia Julai navuna. Hata hivyo siri ya tangawizi si lazima nivune Julai, naweza nikaiacha kwa mwaka mzima, itategemea kama nina soko. Tangawizi unaweza ukaiacha chini ya ardhi kwa mwaka mzima na ikakusubiri upate soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba niseme ukweli kuwa wakulima wa tangawizi ambao tuko Madaba na tuko wengi tunalima tangawizi kwa wingi na sisi hiki kiwanda ni faida kwetu kwa sababu kile kiwanda kitachukua tangawizi ya nchi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine lazima tujifunze, hiki kiwanda kikubwa kilichoko Nigeria ni mali ya Serikali. Ni Serikali ya Kaduna imekijenga sasa lazima sisi tujipe big up, tumeanza wananchi, mimi kama Mbunge nimetoa lile wazo, wananchi 613 wakachangia shilingi 6,000, Rais Kikwete akaniunga mkono kwenye fund raising tukapata shilingi milioni 301, Halmashauri ikaniunga mkono na sasa LAPF inakuja inatuunga mkono hapo ni lazima tuone kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi inafanya vizuri. (Makofi

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumalizia, sitaki kuogongewa kengele. Kwa moyo uliopondeka na kwa unyenyekevu mkubwa niishukuru LAPF, nawashukuru sana na huko walipo wajue wameitendea nchi, hawakumfanyia mtu, wameifanyia nchi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa unyenyekevu mkubwa nakushukuru kwa dakika ulizonipa, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI amesaidia hili kuwezekana namshukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Wizara ya Kilimo. Kilimo kwangu mimi ni Wizara mama kwani wazazi wangu walionipa maisha haya wamenilea na kunisomesha kwa kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi wote wa Tanzania kuanzia vitongoji hadi Taifa na Watanzania wote kwa ujumla tunapaswa kujiuliza swali hili, ni Tanzania ipi tunayoitamani? Jibu sahihi ni Tanzania yenye nguvu ya kiuchumi. Ili Tanzania ifikie kuwa Taifa la uchumi wa kati na Tanzania ya viwanda ni lazima na muhimu kupanua wigo katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yangu ya leo ya Wizara ya Kilimo, nitaongelea suala moja tu nalo ni zao la tangawizi. Nianze kwa kuuliza swali ambalo nitalijibu sawia. Tangawizi ni zao gani? Ni zao ambalo ni jamii ya viungo (spices). Pili, tangawizi ni malighafi ya kutengeneza madawa ya binadamu, vipodozi, vinywaji na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea tangawizi kiulimwengu, Afrika na Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiulimwengu; ukisoma vitabu vya zao la tangawizi ulimwenguni utaona kwamba mataifa tano bora yanayoongoza ulimwenguni kwa kulima zao la tangawizi ni India, China, Nepal, Nigeria, Thailand. Nchi hizi tano bora kwa kilimo cha tangawizi zimeweza kujiboresha kiuchumi kupitia zao hili la kilimo. India inalima asilimia 34.6 ya tangawizi yote inayolimwa duniani, inaongoza kwa kulima tangawizi na pia inaongoza kwa kuitumia. China inalima asilimia 19.1, Nepal inalima asilimia 10.1, Nigeria inalima asilimia 7.8, Thailand inalima asilimia 7.8. Nchi nyingine zinazojitahidi ni Indonesia, Bangladesh, Japan, Cameroon na Taiwan hizi zinaingia kwenye kumi bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisiishie hapo nchi tano ulimwenguni zinazoongoza kwa ku-export tangawizi aidha ikiwa mbichi (raw ginger) au ikiwa imesindikwa, kwa takwimu hizi za mwaka 2015 China inaongoza kwa ku-export asilimia
39.9 ya tangawizi yote iliyouzwa duniani, India inashika nafasi ya pili kwa ku-export asilimia 14.5 japo inaongoza kwa kulima tangawizi duniani lakini inaongoza kwa kutumia tangawizi pia. Nigeria inashika nafasi ya tatu kwa ku-export tangawizi duniani na ina-export asilimia tisa ya tangawizi inayofika kwenye soko la duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa moyo wa unyenyekevu mkubwa, kwa moyo uliopondeka nitoe shukrani zangu za dhati kwa wafuatao:-

Bodi ya Wadhamini wa LAPF na Mkurugenzi wa LAPF kwa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli katika jitihada zake za kuijenga Tanzania mpya ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, LAPF wameingia ubia na kiwanda cha kusindika tangawizi cha Miamba Same Mashariki kupitia kampuni yake ya Mamba Ginger Company Limited. LAPF kuingia ubia na kiwanda cha kusindika tangawizi kuna yatokanayo yafuatayo:-

(i) Walima tangawizi wa Wilaya ya Same na Tanzania nzima watapata soko la uhakika la kuuza tangawizi yao.

(ii) Ni dhahiri kwamba kilimo cha tangawizi Tanzania kitapanuka na haswa kama Serikali itajali kujenga miundombinu endelevu kwa wakulima tangawizi.

(iii) Ni dhahiri kwamba tangawizi sasa tutaingia kwenye biashara ya uhakika ya kuuza tangawizi nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika na haya ninayoyasema kwamba walima tangawizi wa Tanzania wanapata taabu sana inapofikia kwenye kupata soko la zao kwa walanguzi ambao wanawapangia bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangawizi inastawi sana Same Mashariki na mpaka sasa hivi ninapoandika hotuba hii ardhi ya Same Mashariki ililimika tangawizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tunayo mikoa yenye ardhi nzuri sana yenye rutuba kama ile ya Nigeria. Mvua ya kutosha, climate condition nzuri; mito isiyokauka. Mikoa hiyo kwa uchache wake niitaje ni pamoja na Ruvuma, Mbeya, Iringa, Rukwa, Kigoma, Arusha na Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangawizi sasa hivi imeonesha mwamko wa Watanzania kuanza kulima zao la tangawizi. Napata simu nyingi sana kutoka Kigoma wananchi wakinipa simu kuhusu wapi wanauza zao lao la tangawizi. Songea vijijini Jimbo la Madaba wananchi wameanza kilimo cha tangawizi tangu mwaka 2012. Mimi nahamasisha sana kilimo cha tangawizi nami nikiri kwamba nimewekeza katika kilimo cha tangawizi na nimeanza na ekari 20 nalima tangawizi Madaba, Songea Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naisihi sana Serikali ifanye kila jitihada kuliangalia zao hili la tangawizi kwani iwapo Serikali itajihusisha kikamilifu tutakuwa tunatengeneza zao litakaloweza kutuingizia fedha za kigeni. Leo hii nchi ya Nigeria inachangia asilimia tisa ya tangawizi yote inayouzwa kwenye soko la dunia na matumizi ya tangawizi kiulimwengu yamepanda kwa asilimia takriban asilimia 7.5
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kuhusu uvuvi haramu. Tunapata matatizo makubwa kama nchi kuhusu nyavu za kuvulia ambazo si rafiki kwa samaki zinazopelekea kuzaliwa uvuvi haramu. Niende mbele zaidi kwa kusema nyavu hizi ambazo si rafiki kwa samaki ni mara nyingi zinakamatwa na kuteketezwa lakini tatizo hili la nyavu haramu halijapata kamwe kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali kwa kuwa wananchi wetu wanazipenda sana hizi nyavu na kupelekea wao kuingia hasara za mamilioni ya fedha kwani pindi wanapokamatwa zinateketezwa na kwa kuwa hawakomi wanaendelea kuzitumia kinyume na maelekezo ya Serikali. Basi sasa ni vyema Serikali yenyewe ichukue jukumu la kuingiza nchini nyavu za kuvulia na pia Serikali ichukue jukumu la kumiliki viwanda vya kutengeneza nyavu ili tuondokane na kuteketeza nyavu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyavu zinazoteketezwa ambazo ni haramu tunateketeza mabilioni ya fedha za wavuvi ambao ni Watanzania tunavuruga uchumi wa nchi.

Namalizia kwa kusema nyavu za kuvulia ziwe chini ya Serikali yenyewe, Serikali ihusike na utengenezaji na uagizwaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kushukuru kupata nafasi hii ya kuongea. Naomba niseme neno dogo kidogo, hata unapoamua kumnyonga mnyonge lakini mpe haki yake. Serikali ya Chama cha Mapinduzi Awamu ya Tano inafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuzungumze kwa takwimu, tuwe tunazungumza kwa takwimu. Kwanza nazungumzia Kamati ya Nishati na Madini, nazungumzia upande wa madini sasa. Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa Rais Magufuli imefanya mambo makubwa mawili na mambo haya yamewavutia Madiwani wengine wanakuja wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza kudhibiti madini yasipotee na jambo la pili ni upande wa ukusanyaji wa pesa za madini. Serikali ya CCM ya Awamu ya Tano kwa kipindi hiki cha mwaka 2017/2018 nusu tu tuhatujafika mwaka 2018, Serikali imekusanya asilimia 80.4 ya makusanyo ya mwaka mzima. Lengo ilikuwa mwaka 2017/2018, Serikali ikusanye bilioni 194.397 hadi Mwaka 2018 Desemba lakini Serikali hii imekusanya bilioni 156.311 sawa na asilimia 80, sasa utasema hiyo Serikali inacheza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, msiwasikilize hawa, tumewazoea, sisi tunaangalia kazi inayofanywa na wananchi angalieni vizuri Serikali ya Awamu ya Tano inachapa kazi. Ningeshangaa sana Serikali inavyochapa kazi iungwe mkono na hawa, ningeshangaa, lazima hawa wakasirike. Kwa hiyo, msipate tabu Waheshimiwa Wabunge, twendeni kazini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, twende kwenye suala la REA, nipongeze Bunge la Kumi ndilo lilikuja na hii tozo ambayo imeleta manufaa kwa nchi yetu. Naomba nikubali kwamba jambo lolote linapoanza lina changamoto, huwezi kuanza jambo mara ya kwanza ukalifanya kwa asilimia 100, mara ya pili ukalifanya asilimia 100, kidogo kidogo REA itasimama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe takwimu, mwaka 2008 umeme vijijini ulikuwepo kwa asilimia 2.2 tu kabla ya kuwa na REA. Ilipofika 2015 umeme vijijini ukafikia asilimia 21.02, hayo ni madogo jamani? Serikali inachapa kazi, sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 mpaka Desemba, 2017 angalieni Serikali ya Awamu ya Tano inavyochapa kazi, umeme vijijini umefikia asilimia 49.5. Sasa najiuliza hivi hamuyaoni hayo, wenzetu mna macho gani, tafuteni miwani. Serikali inachapa kazi jamani Wabunge wa CCM tujivune. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri Subira Mgalu, anajitahidi sana. Wiki iliyopita alikwenda Kilimanjaro, nampongeza sana, kuangalia matatizo yaliyotokana na REA I na REA II. Kwa hiyo, Serikali inafahamu kwamba kuna changamoto, alikwenda Mwanga, Rombo na akaja Same.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemshangaa, Kata ya Vulha, Kata ambayo Mawaziri wachache sana wanafika, amefika Subira. Kule kuna mradi wa REA II, nilipambana nayo sana ile, Serikali ikapeleka umeme kule lakini haikumaliza. Mheshimiwa Waziri amekwenda kuangalia na amekwenda kuwahakikishia wananchi kwamba REA III inakwenda kumalizia, Serikali inafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Waheshimiwa Mawaziri, Waziri wa Nishati pamoja na Naibu Waziri mlikwenda Kilimanjaro lakini kuna Wilaya ina matatizo sana naomba nisimame hapa niiombee umeme kule ambapo haujafika, Wilaya ya Siha. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Siha kuna Kata moja ambayo ina vijiji vinne, hiyo Kata inaitwa Donyomurwakna. Kuna vijiji vinne kwenye kata hii, vijiji viwili vina umeme na vijiji viwili bado umeme haujafika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kitu kimoja, waacheni hawa, hakuna Serikali ambayo inaweza ikafanya mambo yote kwa wakati mmoja, haipo duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiombea Wilaya yangu ya Siha kwamba vile vijiji ambavyo Mheshimiwa Waziri nimekuletea kimaandishi uhakikishe vinapata umeme na Alhamisi ya wiki hii nahamia Siha. Naomba Watanzania wawe na uhakika kwamba Siha litakuwa Jimbo la Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwahakikishe Watanzania kwamba CCM inashinda Siha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2019 (Toleo la Kiingereza).
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba ku-decalre interest kwamba mimi ni mwananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Wilaya ya Same lakini mimi pia ni mwananchi wa Mkoa wa Dodoma, Jimbo la Mtera. Kwa niaba ya walima zabibu, ndugu zangu Wagogo, nitoe shukrani za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo ametugusa wakulima wa Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiri kabisa tulikuwa tunapata shida sana. Niseme ukweli, mume wangu ni mkulima mkubwa wa zabibu, ana ekari 11 pale Chinangali. Nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa unyenyekevu mkubwa, Bunge lijalo la Bajeti uje Chinangali uone ni kiasi gani wakulima wa zabibu pale tuna shida. Serikali kwa hili mlilolifanya la kupunguza huu ushuru wa mchuzi wa zabibu mmewapa usingizi wakulima wa zabibu hapa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ulivyozungumza, mwaka 2018 zabibu zilioza, zabibu ni zao tofauti na nazi na mazao mengine. Siku ya kuvuna ikifika usipovuna ndani ya wiki moja unapoteza kabisa. Wakulima wa zabibu kwa Mkoa wa Dodoma, including mume wangu, Mzee Malecela, mwaka 2018 tulipoteza moja kwa moja. Kwa hiyo, kwa unyenyekevu mkubwa nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo ametufikiria sisi wakulima wa zabibu.

Mheshimiwa Spika, sina mengi ya kusema, nashukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii ya pili kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na Ofisi yake. Nitachangia maeneo matatu tu. Nitaanza na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, nitakuja Wizara ya Afya na mwisho nitamalizia Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nitakalolizungumza, nafikiri ni jambo ambalo linamgusa kila Mbunge hapa ndani na nina uhakika linamkera kila Mbunge hapa ndani; suala la kuchoma nyavu za kuvulia samaki. Kwanza naomba niipongeze Serikali sana. Serikali inafanya kazi nyingi, inafayanya kazi nzuri sana na Watanzania wanaridhika na mwenendo wa ufanyaji kazi, kwa jinsi ambavyo Serikali inafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la uvuvi haramu, linanipa taabu kidogo. Wavuvi ni wafanyabiashara. Wanapokwenda kuvua na nyavu zao, mtaji wao ni nyavu zao. Suala linalonisumbua kwenye Serikali, jamani Serikali naomba mnisaidie, wavuvi hawa wananunua nyavu madukani. Wao ndio watumiaji wa mwisho. Wanapotumia kuvua wanakamatwa na zile nyavu ambazo zinazaa uvuvi haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu najiuliza kila wakati, kwani hizi nyavu wamezipata wapi? Suala linalonisumbua, hizi nyavu wamezipata wapi? Kikatiba Serikali Kuu ndiye anayetakiwa asimamie maendeleo ya wananchi. Aangalie wananchi wanavyopambana katika kujitafutia maendeleo. Serikali Kuu inatakiwa ihakikishe wakulima wanapata pembejeo, wanapata mbolea lakini mbolea sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inashindwaje kutafuta chanzo cha nyavu hizi ambazo ndizo zinazozaa uvuvi haramu? Swali liko hapo, kwa sababu mvuvi yule kwa ufahamu wangu mdogo, maana yake kule kwetu Same sisi hatuko kama watu wa kwenye Ziwa Victoria. Nina imani kwamba mvuvi anakwenda kununua nyavu, lakini nina uhakika Serikali inapaswa kuangalia zile nyavu kama ambavyo inaangalia pembejeo na mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inanisumbua. Inakuwaje Waziri wa Mifugo anakwenda Ziwa Victoria, anakuta nyavu zilizotumika Ziwa Victoria asilimia 90 ya nyavu zile eti ni haramu? Zinatoka wapi hizi nyavu? Hawa wavuvi wanatengeneza wenyewe? Ndiyo kitu kinanisumbua. Naiomba Serikali sasa kwa sababu hili la kuchoma nyavu za wavuvi, kwanza tunachoma mtaji wa mvuvi yule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mfanyabiashara, ukinichomea mtaji wangu unaniua mimi. Naiomba Serikali ifanye kila njia idhibiti nyavu hizi ambazo ndiyo zinazaa uvuvi haramu. Iangalie hizi nyavu kule zinakotengenezwa; ina maana Serikali haijui nyavu zimetoka wapi? Kama zinaingia kwenye nchi kutoka nje, kwa nini inaruhusu nyavu ambazo zitazaa uvuvi haramu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naona tusikimbilie kuchoma hizi nyavu zikiwa kwa mtumiaji wa mwisho.

Tuziwahi hizi nyavu zinapoingia nchini. Nafikiri Serikali imenielewa. Tutamwonea mvuvi, unless kama hawa wavuvi wana viwanda vyao wenyewe vya kutengeneza hizi nyavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itakapokuja kutujibu, itoe jibu ambalo litatatua hili tatizo. Mwisho kabisa, tusisikie nyavu zinachomwa. Tusikie huko kwenye viwanda vya hizo nyavu au huko bandarini, nyavu zinarudishiwa huko huko. Nimeeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili linahusu Wizara ya Afya. Mimi ni mwanamke ambaye nimepata watoto mara nne. Nashukuru kwa Sheria ya Nchi yangu kila nilipopata mtoto nilipata Maternity Leave ya siku 84. Namshukuru Mungu kwamba nilizaa watoto wangu salama. Sasa sheria ya nchi hii kwenye Maternity Leave iko sahihi, unajifungua mtoto, unapata siku 84 za kumwangalia mtoto mpaka anapata nguvu na wewe unarudi kazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sheria iangaliwe upya, kwa sababu kuna mwanamke anazaa watoto wawili, kuna mwingine anazaa pacha watatu, kuna mwingine anazaa pacha wanne, kuna mwingine bahati mbaya anazaa mtoto mwenye kichwa kikubwa, kuna mwingine anazaa mgongo wazi, watoto hawa wanahitaji uangalizi wa zaidi ya siku 84. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu aliyepata mtoto mmoja, tena mwenye afya ni tofauti sana na mtu aliyezaa kitoto njiti. Ni tofauti na mwanamke aliyezaa mtoto ambaye mgongo uko wazi. Ni tofauti na mwanamke aliyezaa mtoto mwenye kichwa kikubwa, anahitaji uangalizi wa zaidi ya siku 84. Naiomba Serikali ikaingalie hii sheria upya kuliko inavyo- generalize kwamba kila mwanamke akijifungua, 84 days anapumzika. Je, wale waliozaa njiti? Je, ambaye Mungu amempa watoto wanne? Je, ambaye amepewa watoto wawili, wameungana na wana matatizo kichwani? Siku 84 hazitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali, turudi tuangalie hii sheria upya tena kwa uharaka, maana yake juzi nimemwona yule mwanamke aliyetoka pale Aga Khan, amejifungua watoto watatu na ameajiriwa na Serikali hii iliyopo madarakani, hii Serikali yetu. Hivi huyu siku 84 na watoto watatu hawa zinamtosha? Hapo nitaomba Serikali iangalie vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi kwenye Wizara ya Ardhi. Hapa nazungumzia Kata ya Ndungu. Hii kata iko Wilaya ya Same. Mimi naishi next door na Kata ya Ndungu. Kata ya Ndungu ni kata yenye population, tukienda kwenye sensa ya mwaka 2012, population yake ni wananchi 16,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kata, nakwenda kwenye ardhi kwa sababu kwa vipindi viwili nimekaa hapa Bungeni nikitetea wananchi wa Jimbo la Same Mashariki. Hili suala nilikuwa naliongea, kwamba nusu ya ardhi ya Kata ya Ndungu, ardhi yake ina mwekezaji sijui wa mkonge lakini ule mkonge hauendelezwi. Nililalamika hapa Bungeni, Waziri wa Uwekezaji wa kipindi kile Mheshimiwa Mama Maria Nagu, akaja akaona ile shida, akaona kwamba kwa kweli pale kuna tabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 60 ya wananchi 16,000 ni vijana, hawana ardhi, hawana mashamba, hawana makazi, ardhi yote iko kwa mwekezaji ambaye ule mkonge hauendelezi, upo tu. Namsihi Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, yupo Mheshimiwa Mama Angelina, aje Ndungu akaione ile ardhi ambavyo iko pale, hakuna kinachotokea, vijana wa Kata ya Ndungu hawana nyumba, wanaishi na wazazi wao. Anaoa mke, anakaa na mama yake na baba yake. Ndoa itavunjika ile; gubu la mama mkwe! Anataka ajenge nyumba yake, hana mahali pa kujenga. Mkonge umekufa, nusu ya ardhi ya Kata ya Ndungu. Nafikiri Serikali imenisikiliza. Sikuwa mtata sana, nimeeleweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi kuchangia Wizara hii muhimu, Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme ukweli, nimekuwa hapa Bungeni tangu mwaka 2000. Tumekuwa tuna migogoro mingi sana ya ardhi kuanzia mwaka 2000 mpaka sasa hivi ni mwaka 2018. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri Lukuvi, amepunguza migogoro ya ardhi kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme ukweli Mheshimiwa Waziri William Lukuvi, anachapa kazi sana. Anafanya kazi kubwa sana, lakini sio kwamba achukue sifa zote peke yake, ana mke wake ambaye anamwangalia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka Mkoa wa Kilimanjaro. Mkoa wa Kilimanjaro una wilaya saba. Ndani ya wilaya saba, Wilaya ya Same iko hapo ambayo katika ardhi inachukua takriban asilimia 40 ya ardhi ya Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wilaya ya Same asilimia 68 iko milimani, asilimia 32 iko tambarare. Tuna matatizo makubwa mawili ambayo ndiyo yamenifanya nisimame hapa, Nianze kwa kusema kwa Mheshimiwa Waziri; Same tunamwita aje aone matatizo yetu. Haya matatizo ni matatizo yako sehemu kubwa katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kata mbili, Kata ya Makanya ambayo iko Same Magharibi, kata hii tangu mwaka moja elfu mia tisa, kwanza population ya Kata ya Makanya ni takriban wananchi 15,000 kwa sensa ya mwaka 2012. Kwa hiyo, ni Kata yenye watu wengi sana. Kuna tatizo kubwa sana la ardhi pale kwenye Kata ya Makanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna haya mashamba ya mikonge ambayo watu wengi tunayalalamikia kwamba yame-end up kutokuwa na tija kwa wananchi kwenye kata zetu. Kata ya Makanya ni kata yenye matatizo ya mafuriko ya mara kwa mara. Lile eneo zuri kwenye Kata hii ya Makanya ndilo eneo ambalo lina mkonge, la mwekezaji ambaye simjui ni nani lakini ni mwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 1994, wakati huo Waziri wa Ardhi akiwa ni Mheshimiwa Edward Lowassa, kama sikosei, wananchi wa Kata ya Makanya, Kijiji cha Makanya walileta maombi kwamba wapatiwe ardhi takriban hekta 30, kwa sababu ile ardhi wanayoishi wao ndiyo ardhi ambayo ina mafuriko mara kwa mara. Kwa hiyo, hili tatizo ni kubwa sana kwa Kata ya Makanya. Mheshimiwa Waziri, namnyenyekea, aje aione kata ile, aone wananchi wanavyoteseka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, hawana eneo la makazi, pili, ukiangalia kama unatokea Hedaru kwenda Same ardhi kbwa ya Makanya huku kando ya barabara ni kilimo cha mkonge. Vijana wa Kata ya Makanya nao wangependa kufanya biashara kandokando ya barabara ya lami, lakini kandokando ya ile barabara ya lami kuanzia Makanya mpaka Same ni mashamba ya mkonge ambayo nina uhakika hayana tija kwa wananchi wa Kata ya Makanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimetumwa na wananchi wa Same nimwite Mheshimiwa Waziri aje Same na mimi nitakuwepo Same. Tuzunguke Kata ya Makanya aone ni kiasi gani wananchi wa Kata ya Makanya, Same ya Magharibi wanapata adha kwa ajili ya yale mashamba ya mkonge. Mheshimiwa Waziri nafikiri message ameipata vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Makanya ni kata ambayo mara kwa mara Watanzania mnasikia mafuriko, ni kwa sababu ardhi ile ambayo ni nzuri ndiyo yenye mkonge na ardhi ambayo ina mafuriko ndiko wanakoishi wananchi. Mheshimiwa Waziri nimalizie hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi Kata ya Ndungu. Tangu Bunge zima la Kumi nimekuwa nalalamikia Kata ya Ndungu. Kata ya Ndungu asilimia kubwa ni mashamba ya mkonge pia; vijana wa Kata ya Ndungu hawana sehemu ya makazi, hawana sehemu ya biashara, ni mashamba ya mkonge. Mheshimiwa Waziri, nimemwona anazunguka Tanzania, anafanya mikutano mpaka saa sita usiku; namsihi aje kwetu Same, tunamsubiri, tunamsubiri atapata zawadi ya mpunga, atapata tangawizi, aje aone matatizo ya ardhi, mashamba ya mkonge yametuzidi, lakini hayana tija kwa Kata ya Makanya na Kata ya Ndungu. Karibu Same tunakusubiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kukumshukuru Mungu kwamba nimeweza kusimama katika Bunge lako Tukufu ili niweze kuchangia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambayo ipo mbele yetu. Naomba nikushukuru na wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia, lakini nimshukuru sana na nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu, ametoa hotuba nzuri iliyosheheni miradi mingi ya maendeleo, iliyofanywa na Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli ukianza kusema kazi zilizofanywa na Awamu ya Tano utamaliza siku tatu unazungumza tu. Kwa hiyo, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano, nampongeza Rais na Mawaziri wote na Wakuu wa Mikoa, nchi inasonga mbele. Naona kila mtu ana mtazamo wake katika mambo. Baada ya Rais kufanya mambo mengi sana, kuna jambo sasa hivi ameamua kama mnaangalia mambo vizuri, ameamua kuweka misisitizo kwenye uwekezaji. Kwa nini nasema hivyo? Mheshimiwa Rais ameangalia vizuri akaona uwekezaji ndani ya nchi haujakaa vizuri, akaamua kuteua Waziri wa Uwekezaji, Mheshimiwa Angella Kairuki ambaye mimi namwamini sana, amempa Wizara hii na ameiweka chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwa nini ameweka msisitizo kwenye Wizara hii ya uwezekezaji? Dira ya nchi yetu ni kwamba ifikapo 2025 tuwe tumefikia kuwa kwenye Taifa ambalo ni la uchumi wa kati, lakini tuliangalie Taifa la uchumi wa kati na tulipo. Ili tufikie kwenye uchumi wa kati, tunahitaji tuboreshe viwanda kwenye nchi yetu, lakini viwanda tutaviboreshaje, lazima tusimame imara kwenye uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, ili Rais asisitize zaidi katika uwekezaji amewaita Mabalozi wote Ikulu akafanya dhifa, akala nao chakula, lakini akatoa tamko kwa wale ambao mnasomasoma magazeti, kwamba ni mwaka 2019 ni mwaka wa uwekezaji. Mheshimiwa Rais alizungumza kwa wale Mabalozi, lengo lake ni kwamba Mabalozi wote wachukue tamko lile kwenye nchi zao kwamba Tanzania imeamua mwaka 2019 ni wa uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, naomba dakika zangu zote nichangie kwenye uwekezaji. Mimi ni Mwalimu ndugu zangu na Walimu tunaamini unafanya vizuri ukisimamia specialization. Nisingependa kuzungumza mambo mengi sana nitazungumzia uwekezaji na nitachangia kwa maandishi pia nikizungumzia uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, naifahamu nchi yangu vizuri na nimekuwa Bungeni hapa kwa muda wa kutosha. Tumezungumza sana kuhusu pamba na naomba Waheshimiwa Wabunge wanaolima pamba mnisikilize kidogo. Tumezungumza sana kuhusu zao letu la pamba, lakini nikiri bado hatajatumia pamba vizuri kwenye nchi hii. Kuna mikoa minne mikubwa inayolima pamba, Mkoa wa kwanza Simiyu, Mkoa wa pili Shinyanga, Mkoa wa Tatu ni Mwanza pamoja na Geita na wengine wanajaribu jaribu, lakini hii ndio mikoa minne inayolima pamba vizuri. Ukiangalia Mkoa wa Simiyu ukisoma vizuri utaona, Simiyu pekee inalima zaidi ya 40% ya pamba inayolimwa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, hapa nimezungumzia pamba ndani ya nchi, twende kwenye zao la pamba Tanzania katika Afrika na pia twende kimataifa. Tanzania katika kilimo cha pamba ni namba nane, inachukua nafasi ya nane katika nchi 30 za Afrika zinazolima pamba. Hiyo ni upande wa Afika, lakini Tanzania katika kulima pamba Tanzania inashika nafasi ya 22 duniani katika nchi 77 zinazolima pamba. Kwa hiyo, tunaweza Watanzania tukajipambanua kwamba tunalima pamba. Kama dunia nzima nchi zinazolima pamba zipo 77, Tanzania tunashikika nafasi ya 22; kama Afrika zipo nchi 30, Tanzania tunashika nafasi ya nane Waheshimiwa hatulimi pamba? Tunalima pamba.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kama Mbunge mzoefu kusema bado hatujatumia zao za pamba vizuri. Nilipomsikia Mheshimiwa Rais ametangaza 2019 ni mwaka wa uwekezaji, naomba Serikali waende wakajitikite kwenye kuwekeza kwa kutumia zao la pamba, kwa nini nasema hivi? Kwa sababu kuna nchi ndogo hapa Asia inatiwa Bangladesh, mnaifahamu, Bangladeshi hana umaarufu katika kulima pamba hata kidogo, soma vitabu vyote hana, lakini Bangladesh anaongoza kwa kuwa na textile Industry, anaongoza kutuvisha watu wote duniani. Mmarekani anauza nguo sana duniani, lakini viwanda vyote vipo huko Vietnam. Bangladesh ni namba one, anatumia pamba ya ku-export, sasa sisi tuko namba 22 duniani, tuko namba nane Afrika, tuna uwezo wa kufanya vizuri kama Bangladesh na kumzidi. Hivyo, ni lazima Serikali na Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji aende akamsaidie Mheshimiwa Rais, hakumchagua kwa sababu nyingine, amemwamini. Uwekezaji ndio utakaotupeleka kufika kwenye Taifa uchumi kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu katika uwekezaji iwapo Serikali wata-invite mataifa mengi kuja kuwekeza katika textile Industry, tutafika mbali, tutakuwa kileleni, tutafika mbali, nina imani kabisa. Naona vibaya kweli kale kanchi ka Bangladesh hakana umaarufu lakini kila nguo unayonunua Marekani made in Bangladesh, Bangladesh, Bangladesh, hawana umaarufu ni kanchi kadogo kenye takribani square mita laki moja hamsini elfu, kitu kama hicho, lakini kanaongoza duniani kwa kutuvisha mavazi ni number one akifuatiwa na China.

Mheshimiwa Spika, niinyenyekee Serikali, sasa ni wakati wa kusimamia uwekezaji, Mheshimiwa Rais amefanya vizuri sana tangu ameanza, jamani kuna ambaye hawatakubali? Rais anafanya kazi nyingi sana, sasa namwomba Mheshimiwa Rais kwa unyenyekevu mkubwa, nampigia na magoti, aipeleke nguvu yake kwenye uwekezaji na uwekezaji huo aende akaitumie pamba ya nchi hii, tutumie pamba ya nchi hii, tutafika mbali sana.

Mheshimiwa Spika, nisingependa kusema sana kwa sababu nataka kusimama kwenye pamba na Mheshimiwa Waziri naomba niseme nachangia nitampelekea faili lenye data akamsaidie Mheshimiwa Rais kazi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono haja na nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze hotuba yangu kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia na kunipa afya nikaweza kuchangia hotuba hii muhimu sasa ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa utendaji wake mzuri sana uliotukuka na uliojaa uzalendo mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yangu hii ninayoitoa Bungeni hapa na pia nitachangia kwa maandishi nitachangia kuhusu hoja moja tu ya uwekezaji ndani ya nchi yangu ya Tanzania. Nimpongeze Rais wangu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kufanya miradi ya maendeleo ya nchi yetu, anamalizia viporo vya tangu Awamu ya Kwanza mpaka sasa Awamu ya Tano. Mungu ambariki sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi kwa Rais, nirudie kumpongeza kwa kuona umuhimu wa uwekezaji Tanzania. Nasema hivi kwa sababu Mheshimiwa Rais ameamua kuiunda Wizara ya Uwekezaji chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, lengo lake likiwa ni kuimarisha uwekezaji nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dira yetu ya Maendeleo inataka ifikapo mwaka 2025 Tanzania iwe imeshafika kuwa nchi ya uchumi wa kati (middle income country). Nchi haitaweza kufikia nchi ya uchumi wa kati bila ya kuwa na viwanda vya kutosha. Rais wetu amechukua hatua nzuri sana
kumteua Waziri anayesimamia Uwekezaji chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambako vilevile tuna Kituo cha Uwekezaji (Tanzania investment Centre) ili kuratibu vizuri juhudi zote za uwekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili alilolifanya katika mikakati yake ya kuboresha uwekezaji ni pale alipomtaka kwamba mwaka 2019 kuwa ni mwaka wa uwekezaji Tanzania. Alitoa tamko hili mbele ya Mabalozi wote wa nchi za nje wanaowakilisha nchi zao hapa Tanzania. Tamko hili la Rais ni la Kitaifa na ni la Kimataifa. Mheshimiwa Rais kutoa tamko hili la kuutambua mwaka 2019 kuwa mwaka wa uwekezaji amewatuma Mabalozi wa nchi za nje kualika nchi zao kuja kuwekeza nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia uwekezaji nchini nikisema yafuatayo. Tanzania tunalima pamba kwenye Mikoa mikuu minne ambayo ni Simiyu; Shinyanga; Mwanza na Geita. Simiyu peke yake inaongoza kwa kulima pamba zaidi ya 40% ya pamba yote inayolimwa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuiangalie Tanzania kwenye kilimo cha pamba ndani ya Afrika na ulimwenguni. Tanzania kwa kulima pamba inashika nafasi ya 8 kati ya nchi 30 za Afrika zinazolima pamba. Tanzania inashika nafasi ya 22 duniani kati ya nchi 77 zinazolima pamba. Katika hali kama hiyo, Tanzania Afrika na duniani tunalima pamba. Pamoja na Tanzania kuwa nafasi nzuri sana katika kilimo cha pamba lakini kuna tunachokosea na hivyo hatupati faida kubwa kiuchumi kutokana na zao hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia muda wote nilio nao kuishauri Serikali kwamba tutumie zao hili la pamba kupata wawekezaji wa textile industry (viwanda vya nguo). Mheshimiwa Rais alipoteua Waziri wa Uwekezaji chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, lengo lake ni kwamba anataka kuboresha uwekezaji nchini. Mimi ni Mbunge mkongwe, namfahamu Mheshimiwa Waziri aliye na dhamana ya Uwekezaji, Mheshimiwa Angellah Kairuki, nimshauri afanye kila jitihada kuhakikisha zao la pamba linapata wawekezaji wa textile industry.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kidogo niongelee nchi ya Bangladesh. Nchi ya Bangladesh ipo katika Bara la Asia. Ni nchi ndogo, ina eneo la kilomita za mraba takribani 148,000. Pamoja na udogo huo, Bangladesh ina population ya watu wapatao milioni 165. Nalinganisha Bangladesh na nchi yangu Tanzania. Tanzania ukiilinganisha kieneo na Bangladesh ni kubwa ina eneo za kilomita za mraba 945,087 na kulingana na sensa ya mwaka 2017, population yake ni milioni 57.31. Nimependa kuilinganisha Bangaladesh na Tanzania kutokana na jinsi ambavyo nchi hii ndogo ya Bangaladesh….
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuunga mkono hoja hii ya Wizara ya Nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 21, miradi ya kuzalisha umeme; mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maji ya Mto Rufiji, megawatt 2,115. Kwanza nianze kusema kwamba naunga mkono hoja ya ujenzi wa mradi huu kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nianze kwa kumshukuru Mungu kutupatia maporomoko ya Mto Rufiji kwa sababu siyo kila nchi imepata maporomoko kama yale. Huku duniani kuna mabwawa makubwa 70 tu na ili bwawa liitwe kubwa linatakiwa liwe na sifa ya kuweza kufua umeme wenye zaidi ya megawatt 2,000. Bwawa letu hili ambalo linajengwa litakuwa na uwezo wa kufua umeme megawatt 2,115 na hivyo kuingia kuwa kwenye sifa ya kuwa mabwawa makubwa 70 duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende katika dunia, katika dunia kama nilivyosema mabwawa makubwa yapo 70, lakini ukienda duniani bwawa la kwanza kubwa liko China; la pili kubwa lipo Brazil na Uruguay na la tatu lipo Brazil. Twende Afrika, mabwawa ni mengi makubwa lakini tuanze bwawa kubwa mpaka sasa hivi linaloonekana ni kubwa ni bwawa lililopo Msumbiji bwawa la Cahora Bassa Dam ambalo linafua umeme kwa megawatt 2,075. Ina maana la kwetu linalojengwa litakuwa kubwa kuliko hili ambalo linaongoza sasa hivi. Bwawa lingine ni Aswan High Dam ambalo lipo Egypt ambalo linafua umeme megawatt 2,100, hili la kwetu ambalo linajengwa Rufiji litakuwa kubwa kuliko hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Ethiopia walianza kujenga bwawa ambalo litakuwa kubwa kuliko yote Afrika, Bwawa la Grand Ethiopian Renaissance. Bwawa hili litakuwa na uwezo wa kufua umeme kwa megawatt 6,000 na lilianza tangu mwaka 2011 likikamilika litatumia dola bilioni 6.4, bado halijakamilika mpaka leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili bwawa linalojengwa hapo katika maporomoko ya Mto Rufiji; ni kweli kelele ni nyingi sana, upinzani ni mkubwa sana katika ujenzi wa bwawa hili lakini naiomba Serikali ya Chama cha Mapinduzi ielewe kwamba hakuna mtu yeyote duniani, hata haya mabwawa yote yaliyojengwa China, Brazil, Uruguay na wapi, si kwamba walijenga bila ya kuwa na changamoto, wote walipata changamoto kubwa sana na wote walipata upinzani, lakini naomba tuelewe kwamba huwezi kufanya jambo kubwa lenye manufaa katika nchi kama manufaa tutakayopata kutoka kwenye bwawa hili tunalojenga usiwe na changamoto, haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yangu kwa unyenyekevu naisihi twendeni bila kusikiliza kelele zozote. Kwanza, ni lazima mwelewe kwamba moja ya tano ya umeme wote unaotumika duniani unatoka kwenye mabwawa haya 70. Sasa sisi tumepata nafasi ya kuwa na bwawa kubwa na sisi tuingie katika kuwa kwenye moja ya tano ya umeme unaozalishwa duniani, tunasikiliza kelele, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasihi sana, changamoto zilizopo tusisikilize kelele kushoto wala kulia, Serikali wasonge mbele kwa sababu kwanza ukiangalia umeme huu wa hydro ni rahisi. Pili huu umeme wa hydro utatusaidia kwa mambo makubwa mawili; kwanza; ajira kwa vijana wetu; pili. tayari tutakuwa na uwezo wa kuwa na uwekezaji mkubwa kwenye nchi hii. Sasa iwapo hatutakuwa watu tunaothubutu Serikali ya CCM, tunaogopa kelele za watu, tutakuwa wapumbavu. Naomba uthubutu huu uliooneshwa na Awamu ya Tano tusikatishwe tamaa na kelele zozote zile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Anne muda umeisha, ni dakika tano.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, nafikiri Watanzania wamenielewa. (Makofi/Vigelegele)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kushukuru kunipa nafasi hii. Pia nimshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye amenipa uhai nikaweza kuwepo Bungeni leo. Naomba niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Same Mashariki kwa unyenyekevu mkubwa kwa jinsi ambavyo walifanya uchaguzi mzuri sana na kuhakikisha wananirejeshea Jimbo langu la Same Mashariki. Nilishinda kwa kishindo tena kwa haki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais kwa mara ya kwanza amesimama imara akahakikisha nchi yetu inafanya uchaguzi kwa pesa zake za ndani. Nafikiri wote tunaoelewa uchaguzi tumekaa kwenye uchaguzi muda mrefu, siku zote tumekuwa tunabebwa na mataifa makubwa, lakini Mheshimiwa Rais kipindi hiki alisimama imara sana akaiheshimisha nchi yetu tukafanya uchaguzi kwa pesa zetu wenyewe. Waheshimiwa Wabunge naomba hili tulichukue kwa uzito sana na tuone kwamba, Rais ametukomboa kwa kitu kikubwa sana. Vile vile nimpongeze pia Rais alifanya kampeni za kutosha. Alizunguka nchi na aliomba kura na akashinda kwa kishindo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo nirudi sasa kwenye hoja iliyoko mbele yetu. Rais ametoa hotuba siku ya kwanza hapa Bungeni, ilikuwa ni hotuba nzito sana. Namuunga mkono katika area tatu ambazo nimeona nizichague; kwanza katika viwanda, pili katika barabara na tatu nitakuja kwenye afya.

Mheshimiwa Spika, nchi yoyote inakua vizuri zaidi inapokuwa na viwanda vya nguvu. Mimi naomba nirudi kwenye Jimbo la Same Mashariki, Jimbo la Same Mashariki sisi tunalima tangawizi kwa muda mrefu. Kwa muda mrefu sana tunalima tangawizi na tumejenga kiwanda cha tangawizi, mnaokumbuka tangu nimeanza kuingia bungeni hapa nazungumzia tangawizi nikasimama na wale wananchi imara tukajenga kiwanda cha tangawizi.

Mheshimiwa Spika, nikiri kile kiwanda kilikuwa ni dhaifu, lakini namshukuru sana Mheshimiwa Mhagama amekuja ziara kwenye jimbo langu akaja mlimani Mamba Miamba kukiona kiwanda kile. Amekuja nikajua ni Serikali imekuja kuona kile kiwanda. Kiwanda kile yeye mwenyewe amesimama imara pamoja na taasisi yake ya PSSSF, ambao wameingia ubia na sisi wananchi tunaolima tangawizi sasa pale Mamba Miamba, sasa pale Mamba Miamba tunakuwa na kiwanda kikubwa cha tangawizi katika Tanzania kwa sababu PSSSF wameamua kuingiza fedha nyingi sana kuwaunga wananchi wangu wa Jimbo la Same Mashariki.

Mheshimiwa Spika, wao wamechukua asilimia 60 sisi tumechukua asilimia 40, lakini ndugu zangu Wabunge hicho ni kitu kikubwa sana. Ina maana kiwanda kile ambacho kitakuwa kikubwa wananchi wangu wataondoka katika umaskini. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, namshukuru mama Jenista Mhagama mno mno, alikuja jimboni kwangu, nilipata furaha sana ambavyo aliwafanya wananchi wangu wakafurahi. Naipongeza sana Serikali kujali viwanda kwa wananchi. Nimeanza tu kusema kidogo, nitakavyokuwa niko hapa ndani nitaongea sana kuhusu hiki kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono suala la ujenzi wa barabara kwenye nchi yetu. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tuangalieni tulitoka wapi tuko wapi sasa hivi. Tulikuwa kwenye barabara kwenye miji mikuu, ukiangalia Dar es Salaam, ukienda Arusha, ukija Moshi, ukija Dodoma, barabara zilikuwa za kawaida mno, lakini mimi nikienda Dar es Salaam na dereva wangu kwa sababu, mimi niseme ukweli mimi naishi Dodoma, kama sipo Dodoma niko Same Mashariki, Dar es Salaam mimi ni mgeni; tukienda na dereva wangu Dar es Salaam sasa hivi inabidi tupate dereva wa kuingia na sisi mjini. Dar es Salaam Rais amesimama imara mno, ameisimamia nchi yetu imara sana. Sasa hivi Tanzania katika Afrika Mashariki, sio kwamba tujisifu tuseme ukweli, tunaongoza upande wa barabara.

Mheshimiwa Spika, tunaongoza upande wa barabara, lakini naomba nizungumze kama mama. Mama sisi tunapokuwa na watoto unawaangalia Watoto wako sana, unamwangalia mtoto wako wa kwanza, unaangalia wa pili, unaangalia wa tatu, sisi tuliozaa zaidi unaangalia wa nne. Kila mtu anapozaliwa, anapoumbwa na Mwenyezi Mungu akija duniani ana kitu amepewa, ana kitu Mungu amempa cha kwake kwamba, huyu nampa kitu fulani. Tumshukuru Mungu amempa Rais wetu silika ya kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rais Magufuli pamoja na usomi wake, amesoma mathematics na kadhalika lakini nadni ya damu yake ni mjenzi, anajenga barabara. Mimi tangu nimekuwa bungeni hapa nimekuwa nae, hiki ni kipindi changu cha tano, yeye ni Waziri wa ujenzi, Waziri wa Ujenzi, sasa ni Rais anaijenga nchi mpaka mimi na Mheshimiwa Mama Sitta tumekaa tukafikiria hivi akiondoka tutafanya nini, lakini Mungu atatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi imejengwa barabara. Mimi najivuna sasa hivi nikiona hata Dodoma yangu inavyofanana. Dodoma inajengwa na Rais Magufuli mno na nampongeza kwa sababu, mume wangu siku moja alisema aah, hivi kumbe kweli hata nikifa kesho Dodoma imekuwa Makao Makuu, alimshukuru Mungu, lakini Malecela anasifu sana, anamsifu Rais mno, naomba umfikishie message, jinsi anavyojenga barabara za Dodoma.

Mheshimiwa Spika, sasa narudi nikwambie hivi TARURA. Sisi Wabunge wengi wa majimbo tunaitegemea TARURA na mimi niko Kamati ya Miundombinu, kuna mgawo wa fedha za kujenga barabara upo 70 kwa 30. TANROADS anapewa 70; TARURA anapewa 30, mimi naona TARURA aongezewe pesa. Waheshimiwa Wabunge wa majimbo simameni imara sana TARURA aongezewe pesa ili wananchi wetu nao wapate barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeshukuru Serikalini. Serikali imeona majiji makubwa, sasa tunaomba Serikali mrudi mtuangalie na sisi ambao tuko vijijini. Vijijini barabara zina hali mbaya sana. Sisi ambao majimbo yetu yako kwenye milima tuna shida kubwa ya barabara, tuna tabu sana ya barabara. Nasema ukweli lazima Wabunge bajeti inayokuja tusimame imara TARURA apewe pesa. Ule mgawo tunaoambiwa ni mgawo wa kisayansi wa 70 kwa 30 TARURA anapata pesa kidogo, Serikali itafute chanzo kingine cha kumpa TARURA pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudi kwenye afya sasa; namuunga Mheshimiwa Rais sana mkono kwa jinsi alivyosimama imara kujenga vituo vya afya. Amesimama imara kujenga vituo vya afya. Sasa ahakikishe vituo vya afya vinatoa huduma kikamilifu, Madaktari watoshe na vyombo.

Mheshimiwa Spika, sasa hapo lazima nirudi kwenye Jimbo langu, mimi nina tarafa tatu. Tarafa ya Ndungu ina kituo cha afya kimoja, nimetoka kuongea na Waziri wa Afya pale. Tarafa zangu mbili za milimani zote hazina vituo vya afya. Rais alipokuja Same nilimlilia nikamwambia wananchi wanakufa. Tarafa ya Gonja kuna kituo cha afya lakini ni cha KKKT ni biashara, wananchi hawana uwezo wa kulipia zile gharama pale. Tarafa ya Mamba Vunta kuna kituo cha afya cha Katoliki ni biashara. Nimekwenda kumlilia Mheshimiwa Waziri sasa hivi pale, nimempigia magoti aje aone jimbo langu.

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa kuunga mkono hoja hii ya hotuba za Mheshimiwa Rais, naipongeza sana Serikali inafanya kazi nzuri lakini naomba mtuangalie na sisi tunaotoka vijijini. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata nafasi. Kwanza naomba nizungumze kwamba, naipongeza sana Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. Tangu Awamu ya Tano imeanza wote tunashuhudia kazi zinazofanywa na Serikali. Nina uhakika wote ambao tuko sobber tunaona kwamba, Serikali yetu ya Chama Cha Mapinduzi inafanya kazi kubwa sana. Naomba nichukue nafasi hii niipongeze na sio mimi na wananchi wangu wote wa Jimbo la Same Mashariki wanapongeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuzungumzia sehemu mbili ambazo zimeongelewa vizuri kwenye mpango, viwanda, lakini pamoja na kilimo. Naomba mimi niviunganishe hivi vitu viwili, viwanda na kilimo. Niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano kusisitiza sana na kutuwezesha kufungua viwanda; viwanda vidogo, viwanda vya kati, viwanda vikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda hivi vyote vinavyofunguliwa Tanzania vinasaidia sana kilimo kwa sababu, vinachukua malighafi kutoka kwenye kilimo chetu, nafikiri hapo nimeeleweka, lakini kuna tatizo kubwa ambalo tusipoangalia vizuri tutakwenda tunajenga viwanda kwa nguvu sana baadaye vitakosa malighafi. Naomba nizungumzie kule ninakokuona, tumejenga kiwanda cha tangawizi, kile ni kiwanda kimejengwa na wananchi na Mbunge aliyekuwepo madarakani wakati huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi tumefika tumeungana na PSSSF ni mbia wa kiwanda cha tangawizi sio kwamba, ameleta mitambo, ni mbia wa Kiwanda cha Tangawizi cha Mambamiamba, naomba mnielewe vizuri ninalozungumza. Sasa hili jambo tuliangalie kwa nchi nzima, kiwanda kile kilipofika pale Same Mashariki nakiri kinakwenda kupanua kilimo cha tangawizi kwa sana. Wananchi watakuwa wana mahali pakuuzia tangawizi tena sio Same Mashariki tu na Same Magharibi watalima mpaka tukija Mlalo watalima, Lushoto watalima, Tanga watalima, kiwanda kiko pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo nililoliona maana kwa sisi viongozi tuwe tunaangalia huku na huku, tutafute kila njia Serikali, Mheshimiwa Waziri Mkuu namnyenyekea, watafute kila njia ya kwenda kuhakikisha miundombinu ya kilimo cha tangawizi inakuwa inayofanya wananchi waweze kulima kile kilimo. Sasa hivi wanaolima tangawizi kule kwangu ni wengi mno, nilianza na kata mbili, nikaja kata nne, sasa ni tarafa tatu zote za jimbo langu, wote wanalima tangawizi; miundombinu ya kilimo imekuwa haiwatoshelezi. Mifereji imekuwa ni midogo, mito imekuwa haina uwezo tena, lakini bado kuna uwezekano wa kuboresha miundombinu ya kilimo kama Serikali ikija kule na kuangalia hali halisi. Kuna sehemu ambazo zinawezekana kuchimbwa mabwawa makubwa wakati wa mvua maji yakajaa, mvua zinapokuwa hazipo mito ikapata maji kutoka kwenye mabwawa yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namnyenyekea Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri wa Kilimo ni mwepesi sana, namkaribisha. Baada ya Bunge hili twende naye kule kwangu akaone hali halisi ya kuboresha miundombinu ya kilimo kwa ajili ya tangawizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi kwenye mpunga ni hilohilo, nina tarafa inayolima mpunga. Tarafa ya Ndungu kuanzia Bendera, Kihurio, Ndungu, Maore ni mpunga, lakini miundombinu ya kilimo imechoka. Sijui kwa majimbo ya wenzangu, lakini miundombinu ya kilimo Same Mashariki, Same Magharibi ni jirani yangu hata yeye ana hilo tatizo. Naomba Serikali itusaidie kuja kutuangalia kwa sababu, bila ya kilimo hata hivi viwanda tunavyovizungumza itakuwa havina malighafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kuzungumza hilo tu. Nashukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza kwa unyenyekevu mkubwa naomba kukushukuru sana kwa kunifanya kuwa mchangiaji wa kwanza wa hotuba hii ambayo ni muhimu sana. Pili, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutufanya wote tuamke salama tuko hapa ndani.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie dakika zangu kumi kuongea kuhusu TARURA. Naomba niiongelee TARURA katika Wilaya ya Same, TARURA ndani ya Same Mashariki, halafu nikipata nafasi nitakwenda mahali pengine kidogo.

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba mpate picha kamili ya Wilaya ya Same. Wilaya ya Same iko ndani ya Mkoa wa Kilimanjaro lakini ndani ya Mkoa wa Kilimanjaro Wilaya ya Same imeketi kwenye asilimia takribani 40 ya Mkoa mzima wa Kilimanjaro. Kwa hiyo, nikiwa na maana kwamba katika Mkoa mzima wa Kilimanjaro wenye wilaya saba, Wilaya ya Same imeketi kwenye asilimia takribani 40, mki-google mtaikuta hapo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Wilaya ya Same ni kubwa sana ndani ya Mkoa wa Kilimanjaro. Hata hivyo, Wilaya ya Same ndiyo inayopata pesa kidogo ukilinganisha na wilaya nyingine. Hapo naona kidogo nimeeleweka.

Mheshimiwa Spika, TARURA haikuanzishwa siku nyingi sana, imeanzishwa tarehe 2 Julai, 2017. Malengo ya TARURA yalikuwa ni kuimarisha uzalishaji, kwamba wananchi waweze kuzalisha lakini mazao yao yafike sokoni. Hata hivyo, nikiwa mkweli TARURA kwa sababu ya upungufu wa pesa zinazotolewa haifanyi kazi ambayo ndiyo lengo la kuanzishwa kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye Jimbo langu la Same Mashariki, dakika siyo nyingi. Same Mashariki niseme ukweli ni jimbo korofi. Serikali fanyeni taratibu za kupitia majimbo yote myatambue majimbo ambayo ni korofi, laini na madogo ili ufike wakati mgawe sawa hizi rasilimali ndogo tulizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Same Mashariki lina tarafa tatu; Tarafa ya Ndungu, hii ni tambarare, tarafa zinazonisumbua sana ni tarafa mbili ambazo ni za milimani, siyo miinuko, ni milimani. Hao wanaoishi milimani wana winter na summer kama Ulaya. Wananchi wanaoishi milimani tatizo lao kubwa, nikiri na naomba Serikali muende huko ni barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara zote za wananchi wangu wa Same Milimani ni za TARURA. Niseme ukweli, TARURA Wilaya ya Same hatupewi fedha, japo wananchi wa Same Mashariki nina uhakika kuwa ni wananchi tofauti na wananchi wengine, kwani wanachimba barabara zao wenyewe. Asilimia kubwa za barabara za milimani katika Tarafa ya Gonja, Tarafa ya Mambavunta kwenye milima mikubwa na wanachimba barabara zao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipindi hiki sikuwa na njia, maana wananchi wa milimani wako kipindi cha mavuno, wanavuna tangawizi; na wa maeneo ya tambarare Tarafa ya Ndungu wanalima mpunga. Barabara za TARURA ambazo ndiyo zingewezesha wananchi kutoa mazao yao kutoka mashambani kufikisha barabara kuu, zote zimekufa. Sikuwa na njia nyingine, ila mimi mwenyewe kama Mbunge niliongea na Mkurugenzi, nikatumia fedha za Mfuko wa Jimbo, nikaweka Mkandarasi. Fedha zile zingenisaidia kwa vitu vidogo vidogo, lakini uone sasa fedha za Mfuko wa Jimbo nimefanya kazi ambayo ingefanywa na TARURA, siyo haki! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimechonga barabara kilometa 93.16. Mpaka sasa hivi ninapoongea hapa, Mkandarasi yule bado yupo kwenye eneo anaendelea kuchonga barabara zile. Zile fedha ningetengeneza matundu ya vyoo, ningenunua madaftari na nini, zote nimeweka mkandarasi. Nimezungumza na Mkurugenzi, maana sikuwa na njia nyingine. Naomba nilete documents za huyo Mkandarasi huko kwako.

Naomba mchukue hizi documents mpeleke kwa Spika. Mpe Spika. (Makofi)

(Hapa Mhe. Anne K. Malecela alimkabidhi pageboy nyaraka ziweze kumfika Mezani kwa Spika)

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, lazima Serikali ipite iangilie haya majimbo. Haya majimbo hayafanani. Zile fedha za Mfuko wa Jimbo ningependa kufanyia mambo madogo madogo ya kuchochea maendeleo, lakini zote nimekwenda. Nimeweka Mkandarasi mwenyewe wakati ni kazi ya TARURA. Kwa kweli hapo sikufurahi sana. Imenibidi nifanye hivyo niokoe maisha ya wananchi wangu. Wananchi wa Same Mashariki waliniheshimu wakanichagua kwa kura nyingi sana, wakamchagua Rais wangu kwa kura nyingi, wakachagua Madiwani, tena siyo kwamba kura zimeibiwa, acheni maneno; na Madiwani wote 14. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilipoona wananchi hawana uwezo sasa wa kusafirisha mazao, nikachukua fedha nilizopewa na Serikali, tena Serikali angalieni vizuri, ongezeni hizi fedha kidogo. Hizi fedha mtuongezee maana mlikuwa mnaangalia na population, wananchi wameongezeka sana, tuongezeeni hizi fedha.

Mheshimiwa Spika, kutokana na nilivyoongea hapa kuhusu ukubwa wa Wilaya ya Same ambayo ni takribani asilimia 40 ya Mkoa wa Kilimanjaro, tuna tatizo sana la upande wa afya. Tuna Hospitali ya Wilaya moja ambayo ipo Same Magharibi, ipo mpakani mwa Wilaya ya Same na Wilaya ya Mwanga. Wananchi wa Same Mashariki wapo mpakani mwa Mkoa wa Kilimanjaro na Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Spika, nawanyenyekea Serikali, nimeshukuru juzi alikuja Naibu Waziri wa Afya, alitembelea lile Jimbo, akatembelea upande wa afya kwa siku mbili, aliona hali halisi. Niinyenyekee Serikali, oneni umuhimu wa kuweka Hospitali ya Wilaya nyingine upande wa Mashariki kwa sababu eneo ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa TARURA, nilisahau kukwambia kitu kingine, nina barabara moja ambayo ni kubwa sana, inatoka Hedaru kwenda Vunta mpaka Miamba. Hii barabara inabeba wananchi takribani asilimia 40 ndani ya Jimbo langu. Hii barabara haipitiki kabisa na ndiyo barabara inayochukua asilimia 40 ya wananchi, lakini imekufa. Barabara hii magari yanapita kwa shida na ndiyo iliyobeba tangawizi yote ya Jimbo langu. Hii barabara naomba isipewe fedha kidogo kidogo na TARURA, TARURA watafute fedha za Mradi wa Maendeleo, zipelekwe kwenye Tarafa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali…

(Hapa kengele ya kwanza ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, hiyo ni kengele ya pili?

SPIKA: Ni ya kwanza.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, tena sasa nasimama vizuri.

Mheshimiwa Spika, Serikali ifanye kazi ambayo ni ya muhimu na ninaomba jibu hapa, mpite mwangalie majimbo yote ya nchi ya Tanzania. Haya majimbo hayafanani. Hayafanani! Huwezi kuzungumzia Jimbo la Same Mashariki ukaja kulinganisha na Dodoma Mjini. Hapana, hapana!

Mheshimiwa Spika, Serikali ni lazima mtuambie, mnatuangaliaje kwenye haya majimbo? Wengine tunateseka, wengine wanastarehe. Sipendi kupiga kelele hivi, isipokuwa naumia. Wananchi wangu ambao hawana hali inayoridhisha, wana hali mbaya sana. Nafikiri Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI amenisikia. Nitaomba nifanye naye ziara tukimaliza hii hotuba, nipite naye kwenye lile Jimbo hata siku moja tu, kama zaidi, si ataugua!

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na pili nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii. Mimi dakika zangu sijui kumi, saba, tano nitaongea kitu kimoja tu, nitaongea kitu kimoja ambacho ni kikubwa sana fedha za miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza sana Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kuanzia Awamu ya Kwanza, Awamu ya Pili, Awamu ya Tatu, Awamu ya Nne, ya Tano hadi hii awamu ya sita, Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inajitahidi sana kupeleka fedha za miradi ya maji kwenye Mikoa kwenye Wilaya kwenye kata hadi kwenye vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongee kitu ambacho naomba Serikali inisikilize vizuri Waziri unisikilize vizuri, miaka ya 1970, 1971,1972 na 1973 nilikuwa msichana mdogo ambaye nilikuwa Sekondari nina akili timamu kuanzia mwaka 1970 hii ilikuwa ni Awamu ya Kwanza, nakumbuka wakati pale kijijini kwetu,ninatokea Same Kata ya Kihurio Kijiji cha Uzambara miaka hiyo ya 1970 hadi 1974 nakumbuka Serikali ilileta mradi wa maji kwenye Kata yangu ya Kihurio, Kijiji cha Uzambara. Mradi ule Mheshimiwa Waziri ulikaa kwa muda mrefu sana kwanini? Serikali ya Chama cha Mapinduzi inapeleka fedha za mradi nyingi sana kwenye Mikoa, Wilaya na Kata lakini wakishapeleka ile miradi wanaachia uangalizi wa ile miradi wananchi ndio waangalie ile miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakumbuka ni vema nifanye comparison mwaka 1970, 1971, 1972 hadi 1980 mradi ulioletwa kwenye Kata yangu ya Kihurio, mradi ulikuwa unaangaliwa na kijana mmoja akiitwa Ally Mabomba, kijana huyo ameajiriwa na Serikali ndiye kila saa 12 asubuhi mnaona maji yanatoka amekwenda kufungua maji kwenye chanzo huko, huko kwenye tenki maji yanapotokea saa 12 jioni Ally Mabomba anakwenda kuyafunga yale maji siku nzima Ally Mabomba anazunguka na Baiskeli kuangalia mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ameajiriwa na Serikali anazunguka siku nzima na baiskeli yake Kijiji kwa Kijiji kitongoji kwa kitongoji anaangalia mradi wake wa maji mahali kuna kasoro anarekebisha yeye. Sasa tuangalie sasa hivi miradi yetu inakwendaje? Serikali inapeleka fedha nyingi sana za miradi nyingi sana, miradi ile inawekwa vizuri inajengewa matenki, wanafanya kila kitu miradi ile ikishaisha kunaundwa kamati ya maji sijui huko kwenye Kata zetu na vijiji vyetu wale ndio wanaoangalia ile miradi kule kwenye Kata.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni Mbunge hiki ni kipindi cha tano na tangu nimekuwa Mbunge kumekuwa na miradi kuanzia bendera, mradi wa kihurio, Mradi wa Ndungu, mradi wa Mahore, mradi wa Kalemau miradi hii inaletwa na Serikali mtakaa miezi sita, saba mradi umeharibika wanaanza kupelekana mahakamani fedha zimeliwa wanaanza kusumbuana huyu ndiye amekula, ile Kamati inayoangalia ule mradi sio, ni kamati wananchi wameichagua wenyewe na ninaona kama Mbunge lakini hakuna mtu mwenye taaluma hata kidogo ya miradi. Sasa nimeomba nizungumzie hili na Waziri unisikilize vizuri tuleteeni fedha za miradi ya maji huko kwenye Majimbo yetu. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ile mkishaiweka vizuri fanyeni kila mahali penye mradi kuwe na mtaalam anayeangalia mradi ule. Ama sivyo Serikali ya Chama cha Mapinduzi mtaendelea kutumia pesa nyingi sana kupeleka miradi ile lakini kwa sababu uangalizi wa ile miradi siyo, inakuwa hamjali tena, mkisha-install mradi wa 20 milioni, kama sasa hivi kuna mradi mkubwa unakuja huko umetokea Same, Mwanga, Korogwe umechukua mabilioni ya pesa mradi ule utakapoingia kwa wananchi naziona pesa ni nyingi sana, mimi kwa sababu nimekaa muda mrefu kwenye Majimbo miradi mingi inakufa sana kwa sababu Serikali hawarudi kuangalia ile miradi. Tunafanya sherehe, mradi tumeanza, tunachinja kuku na ng’ombe baada ya hapo hatuwaoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta tunatengeneza Kamati ya Maji sijui wanakusanya hela wanaiba huko huko, wanagombana huko huko hata koki wanashindwa kutengeneza. Mheshimiwa Waziri mtakuwa mnatuletea pesa ambazo hazitoi matokeo mazuri. Sisi tunawashukuru sana mnapotuletea pesa na mnapoanzisha hii miradi kwenye kata zetu ahsanteni sana lakini rudini muiangalie ile miradi, kila mradi uwekeeni mtu kama yule kaka aliyekuwa anaitwa Ally Mabomba, nimekaa naye kuanzia 70 mpaka 78. Marehemu mama yangu alivuta maji kutoka pale ambapo jumuiya yote tunachota maji akaweka uani yale maji nimeyachota kwa miaka nane sasa hivi hakuna kitu kama hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi nilisimama hapa kuiomba Serikali ya Chama cha Mapinduzi, ahsanteni sana mnatuletea miradi mingi sana lakini mkishaiweka ile miradi wekeni wataalamu wa kuiangalia. Nilikuwa na moja tu la kuzungumza, nashukuru kama Serikali imenisikiliza lakini naomba hili tuliangalie na Waheshimiwa Wabunge huko mliko kwenye Majimbo yenu mhakikishe Serikali ikiweka miradi inaleta wataalam kuangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Vilevile nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri wawili na watendaji wote wakuu wa taasisi ambazo ni za Wizara hii tunayoizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru Wabunge sana. Wabunge wamefanya kazi kubwa sana kuanzia jana. Kazi waliyoifanya ni kazi yao ya Kikatiba. Naomba nikiri, kweli mimi tangu nilipochangia hotuba ya Waziri Mkuu nilizungumzia barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwaambie Serikali kitu kimoja; mnajenga barabara, lakini mnajenga barabara ambazo sizo. Hamjafanya research ya kutosha mkajua barabara zinazostahili kujengwa. Mnarudia barabara zile. Serikali imesoma hotuba hapa, lakini hotuba ambayo Serikali mmeisoma ni ya Serikali; hotuba ambayo inapaswa kutekelezwa na Serikali, ni hotuba inayotoka kwa wananchi hawa; hawa Wabunge ambao ndio wawakilishi wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema Serikali ikajua kwamba wanaozijua barabara hizi ni Wabunge. Wabunge ndio wanaotoka wananchi walipo; Wabunge wanawakilisha wananchi kwenye majimbo yao, ndio wanaozijua hizi barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ukweli, sitaki kusema kwa kirefu, lakini Serikali niwaombe sasa, tena nawaomba kwa mara ya pili; fanyeni kazi kubwa kuanzia kesho, mpite nchi nzima ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mkazijue hizi barabara. Barabara nyingi vijijini hamjazijenga ndiyo maana kumekuwa na kelele mno hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa Wabunge wote waliosema, hakuna kichaa hata mmoja humu. Wote wana akili timamu. Haiwezekani mtu na akili zake timamu atake kucheza karate humu ndani, hapana. Anaogopa 2025 watammeza Wajumbe. Hali ni mbaya sana kwenye majimbo yetu, hasa ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali nawaomba – tena nisiseme kwamba nawaomba, hapana; nawasimamia sasa. Haya ni madaraka yangu niliyopewa na Katiba kwamba niwashauri, lakini wakati mwingine niwasimamie. Hamzijui barabara ambazo mnapaswa kuzijenga. Barabara nyingi sana, zote zilizotajwa na hawa Wabunge hapa, ndizo barabara ambazo zinahitaji kujengwa. Hotuba mliyoisoma hiyo, sasa pateni picha kamili, hotuba ni hii huku. Hii huku ndiyo hotuba. Sisemi lugha tofauti, lugha yangu ni kwamba hotuba mnayopaswa kuiangalia ni hii inayotoka huku sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri nimeeleweka.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika zangu mbili nizungumze kitu kimoja; barabara nimeeleweka…

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. ANNE K. MALECELA: Hapana, dakika mbili bado.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kidogo kuhusu bandari. Tumezungumza sana kuhusu barabara…

NAIBU SPIKA: Sekunde 30 malizia sentensi.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kidogo, ahsante. Amenipa dakika mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumezungumza sana kuhusu barabara, tunaisahau bandari. Bandari ni kitu kikubwa chenye mambo mengi ambalo ndilo lango la uchumi wa nchi hii, lakini bandari tumekwenda tukaiweka ndani ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Tuwe makini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna mfanyabiashara mzuri kama India, lakini mwaka 2020 India ameichukua bandari akaiundia Wizara yake ili aweze kuishika vizuri.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi kuzungumza lakini afya yangu sio nzuri nitazungumza kwa shida, Jimbo langu la Same Mashariki asilimia 99 mfano, wote ni wakulima kwa hiyo wao bajeti yote wanasikiliza Wizara ya Kilimo. Ninamshukuru Mheshimiwa Waziri ninamshukuru Naibu Waziri wote ni wachapakazi ninafahamu, lakini ninaomba niwaambie tatizo langu kubwa, Jimbo la Same Mashariki lina tarafa tatu na katika tarafa tatu tarafa mbili zinalima tangawizi tarafa moja inalima mpunga.

Mheshimiwa Spika, wamelima haya mazao kwa muda mrefu na hayo mazao ndio yanayowafanya nao waishi. Tatizo ambalo liko Same Mashariki ni kwamba kuna tatizo kubwa la miundombinu ya kilimo, miundombinu ya kilimo imekuwa imechakaa sana nikisema hivyo nina maana hawa wanaolima mpunga wanategemea scheme ya kulimia ule mpunga scheme ile imechoka na niseme kweli hili jambo ya scheme yangu ya Kata ya Ndungu nimeliungumza sana na Naibu Waziri na Naibu Waziri nakiri kwamba umeanza kulifanyia kazi nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, lakini tarafa mbili Tarafa ya Gonja na Tarafa ya Mambavuna wananchi wangu wanalima sana tangawizi, na ninaomba niseme kweli katika Tanzania nzima Jimbo la Same Mashariki ndilo Jimbo pekee ambalo wananchi wanalima tangaziwi mno, sasa Mheshimiwa Waziri Jimbo ambalo wananchi ndio asilimia kubwa wanalima tangawizi na wanajitahidi sana. Ninaomba tukimaliza bajeti, ili Bunge la Bajeti Waziri twende wote tukaone hao wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alikuja Rais Kikwete kwenye Kata ya Miamba ambayo Mheshimiwa Mbuge wa Peramiho umekuja juzi alikuja Rais Kikwete mwaka 2014 nikasimama jukwaani nikamlalamikia kwamba Mheshimiwa Rais wananchi hawa wanalima tangawizi vizuri wanashirikiana na Mbunge na tumejengwa na kiwanda cha Tangawizi, miundombinu imekufa nikiri na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Kikwete alitoa shilingi milioni 800 akanipa kusaidia ile miundombinu ya kilimo cha tangawizi hiyo ilikuwa ni Awamu ya Nne, Awamu ya Tano, sikuwa Mbunge kwa hiyo sijui nina uhakika aliyekuwa Mbunge hakuzitafuta fedha kwa hiyo wananchi hawakupata zile fedha, sasa hii ni Awamu ya Sita… (Makofi)

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa Mheshimiwa Naghenjwa Kaboyoka.

T A A R I F A

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, msemaji anaposema sikutatufa fedha wakati alikuwa anasema kiwanda kinafanya kazi ningetafuta fedha ya nini lakini ajue kwamba PSSSF walileta mashine mpya, kiwanda kilichokuwepo kilikuwa ni bomu.

SPIKA: Unapokea taarifa hiyo Mheshimiwa Anne Kilango.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, sipokei huyu mama amechanganyikiwa ninaongelea Kilimo, naongea kilimo cha tangawizi siongei kiwanda amechanganyikiwa naendelea Mheshimiwa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ninachoomba sasa ninakwenda kwenye kazi sizungumzi mambo hayo nakwenda kwenye kazi. Ninaiomba Serikali ya Awamu ya Sita, Serikali ya Awamu ya Nne iliona tatizo la miundombinu Rais akanipa shilingi milioni 800 na aliponipa alisema Mheshimiwa Anne Kilango jitahidi sana kila awamu ikupe fedha za miundombinu Awamu ya Tano sikuwepo Serikali haikutoa. Awamu ya Sita sasa ninaomba kwa unyenyekevu mkubwa Mheshimiwa Waziri tukimaliza Bunge hili ninafunga mizigo yangu ninakuja kukuchukua kwako, twende ukaona hayo matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matatizo ya wananchi wangu ni matatizo yangu mimi, wao wamenituma nije niwasemee mimi sikuja hapa kucheza niwasemee wananchi wangu na leo nimekuambia tangu jana ninaumwa lakini nimekuja ili niwasemehe wananchi wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakuomba Mheshimiwa Waziri Tarafa ya Bonja na Tarafa ya Mambavunda twende mimi na wewe ,tarafa ya Ndungu nitakwenda na Naibu Waziri naomba niseme ninaunga mkono hoja kwa sababu ninajua Mheshimiwa Waziri tutakwenda ninaunga mkono hoja tena sina mahali ninapoleta vuruga na wewe ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii maalum sana, Wizara ya nguvu, Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa na hoja tatu tu za kusema leo; hoja mbili naomba nizungumze hoja za Kitaifa, na hoja moja kubwa nizungumze Jimbo langu la Same Mashariki.

Mheshimiwa Spika, sisi Wabunge tunaishi na Serikali humu ndani. Wakati Serikali inafanya jambo zuri, ni vyema Wabunge tujifunze kuisifu Serikali. Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inayoongozwa na mama Samia Suluhu Hassan, mpaka sasa tuliposimama hapa, inakwenda vizuri sana upande wa Mradi wa Rufiji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu Mradi wa Rufiji Serikali ilipoanza kulikuwa na maneno mengi sana. ukweli naomba niipongeze Serikali kwa kuthubutu. Serikali imefanya kitu ambacho wengi tulikuwa hatukijui vizuri, lakini mpaka sasa hivi Serikali imefanya mradi ambao ni mkubwa kweli katika Afrika Mashariki. Na Mradi huu wa Umeme wa Rufiji katika Afrika Mashariki ni wa kwanza wa kipekee.

Mheshimiwa Spika, ukija katika Afrika nzima, mradi wenye hadhi hii nikiri wa kwanza uko Ethiopia, tukubali; wa pili uko Nigeria; wa tatu uko angola; wa nne uko Tanzania. Tumepiga hatua kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, na ninakumbuka nilikuwepo humuhumu ndani, kulikuwa na migongano mingi nje ya nchi, huko ulimwenguni walisema maneno mengi. Nimpongeze Rais wa Awamu ya Tano, alisimama imara sana, tena alitumia nguvu nyingi sana; Mungu amuweke mahali pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Megawatt 2,113 siyo ndogo. Tanzania na Watanzania wote kwa ujumla tutaona mafanikio makubwa mradi huu utakapokwisha. Mradi huu umefikia asilimia 52. Nimpongeze na Waziri wa Nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, Waziri wa Nishati mwaka 2017 ndio alianza hii Wizara hapa, zilikuwa zipo mbili; Nishati na Madini. Zikatenganishwa 2017, huyu kijana akachukua hii Wizara.

Mheshimiwa Spika, nikiri kabisa na niseme ukweli Mheshimiwa Waziri, ukitembea mtu hasikii hata hatua zako zinavyokwenda, lakini unakwenda mbio sana, unajitahidi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na niseme; sina kawaida ya kusifu Mawaziri, lakini huyu kijana nimeona leo nimwambie ukweli, jitahidi sana, tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine kikubwa; huu mradi tunaujenga kwa pesa zetu wenyewe Watanzania jamani. Huu mradi ni mradi wa trilioni 6.5; hatukukopa mahali, hatukupewa msaada, zote ni pesa za Watanzania. Hivi kwa nini tusijivune? Trilioni 6.5 siyo pesa ndogo, ni hela zinazotaka uthubutu mkubwa. Nawapongeza sana Serikali kwa hilo.

Mheshimiwa Spika, na ninaomba niwaambie ukweli; leo nimeamka vizuri sana.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ninaomba nimpe taarifa Mheshimiwa mama Kilango; ni kwamba kitu kinachofurahisha mkandarasi hadai hata senti tano kwa kazi alizofanya. Kwa hiyo, Serikali imefanya vizuri na Mheshimiwa mama Samia, Rais wetu, anaendeleza gurudumu lilelile. (Makofi/Vigelegele)

SPIKA: Mheshimiwa Kilango, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, tena naipokea kwa unyenyekevu. Mheshimiwa mama Manyanya, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, naomba niseme ukweli; tusipoisemea Serikali yetu vizuri, nani ataisemea? Ni sisi tumeiweka madarakani. Tumepambana tukashinda; Chama Cha Mapinduzi, Serikali inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo nimempenda sana; huu mradi wa kupeleka umeme vijijini. Nilikuwepo tangu mwaka 2000 humu ndani, niliona umeme ulivyokuwa unasuasua, niliona. Nilikata tamaa. Lakini katika vijiji 12,268 vya nchi yetu sisi, leo hii kuna vijiji 10,312 vimepelekewa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata kama umeme umefika kijijini haujaenda vitongojini, lakini ni mwanzo mzuri kwamba umefika vijijini next utakwenda kwenye vitongoji vyetu. Serikali mmenifurahisha sana katika hilo pia, haswa sisi mnaotuona tulio simama hapa wengi wetu tunatoka vijijini, tumezaliwa vijijini, tumekulia vijijini bado tupo vijijini huku tumekuja kutembea sisi ni watu wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, asilimia 86 ya vijiji vyetu tayari wameona umeme, tuishukuru Serikali ya Chama Cha Mapinduzi na ile mikakati Wabunge mlioiweka hapa kwamba chukueni pesa hapa kwenye mafuta pelekeni huku mkakati ule ulikuwa mzuri sana. Ulikuwa mkakati mzuri sana, lakini niseme ukweli mnakumbuka mwaka 2015 ambao mpo sawa tulikuwa namba 39 katika nchi 54 za Afrika tulikuwa namba 39, nikisema hivyo sijui mnanielewa, kwamba katika nchi 54 za Afrika tulikuwa namba 39 kwa kupeleka umeme vijijini. Leo tukizungumza hapa katika Afrika sisi ni namba moja katika kupeleka umeme vijijini, hivi hapa mtasema Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inacheza? Inafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Naomba niipongeze Serikali sana, sasa naomba niachane na Serikali naomba tugombane kidogo na Serikali. Naomba nigombane na nyie kidogo ili mfanye kazi. Nimezungumza kitaifa sasa naenda kwa walionichagua jamani. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri naomba uniangalie vizuri, nimeingia Jimbo la Same Mashariki mwaka 2005 nikawa nasema humu ndani nagombana na Ngeleja, nagombana na Muhongo kuhusu umeme wa Tarafa ya Mambavunda, wananchi wangu wanaishi mlimani sana na wanapoishi kule wanaishi na migomba, na miti, mitangawizi kuna giza sana, nilisema kwa miaka tisa, 2014/2015 Serikali ndiyo ilipoona ikanipa pesa za kupeleka umeme katika Tarafa ya Mambavunda, nikashukuru, nikafurahi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha kwanza nilichokiona kinaitwa Mwala kilipata umeme mwaka 2015 nikafurahi nikaona umeme. Mradi ule Serikali ilisema utakwenda 2015, 2018 utakwisha, wananchi wakafurahi, wakashangilia, leo ni 2021mradi ule 2015 ulikwenda kidogo ulisimama, 2015 ukasimama, 2016, 2017, 2018, 2019 waziri juzi ndiyo umeanza kidogo.

Mheshimiwa Spika, nasimama vizuri kukwambia waziri huu mradi wale wananchi walitegemea sana nao waingie kwenye taa, waingie kwenye mwanga, mliwaacha tangu 2015 mkaenda vijiji viwili,vitatu tu mradi huu mpaka leo nimeanza kwa kuwasifu Serikali narudi kuwaomba tafadhalini huu mradi umalizeni, hawa watu mliwapelekea taa kidogo vijiji viwili, vitatu mradi huu ni wa tarafa nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu mradi ulikuwa uende Vunta, uende Papa, uende Miombo, Uende Mwala, uende Kidandini, uende Mwateni, Njagu, Kirangare, Makasa, Mshewa, Pangani, Vugwamakati, Hedaru, Mweteni, Tambwe, Tintin na cha Nguruwe. Mlikwenda sehemu kama tatu tu, sasa mimi ni Mbunge Same Mashariki kama mlilala hapo katikati sababu siijui, leo nakwambia Mheshimiwa Waziri utoe majibu kwa wale wananchi kwanini ulisimama tangu 2015. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,umerudi kuanzia 2020 hapa mwishoni niliuona nimekwenda mwenyewe naona una wakandarasi kule, lakini wananchi wangu wana wasiwasi kwamba huenda utasimama tena, naomba Mheshimiwa Waziri sitakamata shilingi, lakini uniambie kwanini ulisimama, na utamaliza lini huu mradi.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, sitaunga mkono hoja kwanza. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Naomba nikiri kwamba leo ninasimama kwa unyenyekevu mkubwa kuliko siku zote nilizosimama hapa Bungeni kuchangia bajeti. Kwa nini? Mnaijua sababu. Imeletwa bajeti ya kipekee kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni kipindi changu cha tano, sijawahi kuona bajeti ya sura hii. Hii ni bajeti ambayo ni ya kipee, ni bajeti ambayo imekwenda kugusa Watanzania wote. Hii ni bajeti ya kwanza ya mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Mama Samia ni mama mwenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikwambie kitu kimoja. Mimi ninayeongea hapa ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, ngoja nisimame vizuri; ninayoongea siyo maneno yangu, haya leo nimetumwa na wananchi wa Same Mashariki. Wameniambia nije hapa Bungeni, utanisaidia nipige magoti kidogo niishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi, nimshukuru Mama yetu Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu. Kwa nini? Jamani, sisi tangu tumeanza Bunge hili, kila Mbunge anayesimama, anazungumza TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeizungumza TARURA miaka mingi, jamani TARURA iongezewe pesa, kila Mbunge amezungumza. Sasa tabia ya akina mama iko hivi, mnisikilieze vizuri. Akina mama, hata kama ana homa, amelala kitandani, mtoto akilia, mama ananyanyuka. Anamwangalia mtoto, kwa nini analia? Wabunge mmelia sana. Mama ana kazi nyingi, lakini amenyanyuka. Ana kazi nyingi sana. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumelalamika sana na barabara za vijijini. Mimi ni mhanga wa kwanza ambaye barabara zinanitesa, kumbukeni hotuba zangu kabla ya bajeti kuanza. Maana yake mtoto analia, ana njaa saa saba iko mbali ya chakula cha mchana, hapa katikati unamwambia kula hiki kidogo. Bajeti inaanza Julai, mama akasema jamani nimewasikieni Wabunge na ugomvi wa TARURA, embu chukueni shilingi milioni 500 hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, naomba niwaambie kitu kimoja. Jambo alilofanya mama Samia Hassan, limegusa sana wananchi. Kwangu wamefanya sherehe siku tatu kwa sababu ya barabara. Sasa naomba niwaambie kitu kimoja, mama amefanya upande wake, ametoa kila Jimbo shilingi milioni 500. Waheshimiwa Wabunge, Bunge linakwisha tarehe 30, nendeni majimboni mkazisimamie shilingi milioni 500. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa onyo kwa Mameneja wa TARURA Wilaya, hizi shilingi milioni 500 isipotee hata shilingi moja. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Kabisa! (Makofi)

MHE. ANNE K. MALECELA: Waheshimiwa Wabunge, kasimameni imara. Kwa nini nasema hivyo? Ili tuone kitu mama alichofanya, kionekane kizima kizima, lakini mkiziachia zikidokolewa, mtakuwa mnamuumiza aliyezileta hizi pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wangu wamenituma nisema hayo. Kwa kweli kwa ajili ya wananchi wangu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu tunaomba upumzike sasa. Wananchi sasa umewachanganya. Wananchi wamechanganyikiwa na mapenzi yaliyoota ni makubwa sana.

Tunaomba mwendo huu mlioanza Serikali ya Awamu ya Sita, mwende nayo mpaka mama amalize awamu zake zote mbili. Tunawasihi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa unyenyekevu mkubwa, hili la shilingi milioni 500 Waheshimiwa Wabunge tafadhali, baada ya tarehe 30 hizi safari zenu za Dubai, sijui India, sijui wapi, hapana. Majimboni, tukazisimamie hizi shilingi milioni 500. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa wale ambao hawana matatizo ya barabara hawachanganyikiwi. Naomba niwaulize, tangu tumeanza Bunge hili, kuna hotuba nimesimama nisiongee barabara?

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna. Kero kubwa ni barabara kwenye jimbo langu. Mama yetu amekwenda akagusa wananchi wangu kwenye mioyo. Furaha iliyoko Same Mashariki haijapata kutokea. Sasa naomba nirudi kwa Serikali niwashauri kitu kimoja. Tusichukulie mambo kiutani utani. Let us work!

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kuhusu kukusanya mapato. Ni kweli mnakusanya, lakini tunaposafiri kwenda nchi za wenzetu, tujifunze. Mimi nilikwenda China kabla hawajafunga China. Nikienda China nakaa kama siku 5, 6 au 10. Siwezi kuzunguka China mwenyewe, lazima nizunguke na mkalimani. Nikafika mahali nikawakuta wazee wanauza mahindi. Nikamwambia yule mkalimani, ngoja ninunue mhindi hapa. Akanichukulia mhindi mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize. Nilipopewa ule mhindi, nikaula, nikaupenda. Nimepokea ule mhindi, nimeuweka mdomoni, nikamwona yule mzee anayeniuzia, anaandika kitu kwenye simu yake. Nikamwuliza yule mkalimani, anafanya nini? Akasema analipa kodi. Yaani pesa niliyolipa, tayari analipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, kuna pesa nyingi sana tunaziacha. Tafuteni njia ya kukusanya pesa. Huyu Mchina, mzee mtu mzima, akaja mtu wa pili mimi nimesimama pale, akanunua mhindi. Mzee anatoa mhindi, anaandika. Anakusanya, lakini anakusanya kodi kwa furaha, tena ana raha. Jitahidini mkatoe elimu kwa wananchi, walipe kodi bila ya shuruti. Waone raha kulipa kodi. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kuna jambo kidogo naomba nizungumze tofauti. Hili suala la kulipa kodi kwenye majengo rudini mkaliangalie vizuri Mheshimiwa Waziri. Huko mitaani tusidanganyane, kuna mkanganyiko. Kinachohitajika ni kwamba Waziri mkaliangalie vizuri hili jambo mliweke vizuri kwa wananchi lieleweke, wananchi wawe na raha. Hatupendi bajeti hii ya kwanza ya Mheshimiwa Mama Samia Hassan Suluhu iwe na maneno maneno huko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika, Mheshimiwa Mwigulu nakuheshimu, ukaangalie vizuri, utakapofunga hapa ukijumuisha, Watanzania wakuelewe kwamba hii kodi anayekwenda kulipa ni nani; kati ya mwenye nyumba na mpangaji? Iwe straight inaeleweka, lakini tusiseme kwamba imekuwa rahisi, hapana. Sisi kazi yetu ni kuwashauri nyie. Mitaani hii kidogo imeleta mkanganyiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninapiga magoti tena, nimetumwa na wale wananchi wa Same Mashariki, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, mimi leo nitaongea kwa kifupi, kwanza nianze kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi, nimpongeze Rais Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Kwanza wa Rais, Waziri Mkuu pamoja na Baraza la Mawaziri lote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maendeleo ya nchi yanaletwa na Serikali pamoja na wananchi. Naomba niseme kwamba, kwa kipindi hiki cha Awamu ya Sita mwaka wa kwanza, Serikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya kazi kwa bidii zote sana na sisi tulioko huko Majimboni wananchi wanaendelea kufarijika. Mpaka hapo nafikiri nimeanza kwa kifupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa niingie kwenye jambo ambalo nataka kulichangia kwenye hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Naomba nichangie jambo moja tu, sekta ya uzalishaji, Fungu Namba 37 - Kilimo.

Mheshimiwa Spika, nikiongea kilimo kama Mbunge wa Same Mashariki, zaidi ninakwenda kugusa kilimo cha tangawizi. Nagusa kilimo cha tangawizi kwa sababu, ndani ya Jimbo langu mimi Tarafa mbili zote, Tarafa ya Mambavunda na Tarafa ya Gonja, wananchi wanategemea kilimo cha tangawizi, lakini nikizungumza kwa Tanzania, Tanzania kuna Mikoa ambayo inalima tangawizi sana, Ruvuma inalima tangawizi, ukija Mbeya wanalima tangawizi, Morogoro wanalima tangawizi na Mikoa mingine imeanza kulima tangawizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba kwa Tanzania niachie hapo, sasa nije kwenye tangawizi ulimwenguni.

Mheshimiwa Spika, hili zao sisi watanzania, zao la tangawizi, tunaliona kama ni zao ambalo halihitaji kipaumbele kabisa, naweza nikasema tunalipuuza. Twendeni duniani huko, tuanze na India. India kwa ulimwenguni ni Taifa la kwanza kwa kulima tangawizi, nakiri kwamba, wao hawa- export zaidi kwa sababu wao wenyewe kama India wanakula sana tangawizi, lakini ukiangalia India kwenye soko la dunia anapeleka asilimia 43.81 karibu anafikia asilimia 50. Na hizi data ninazizungumza nazipata August mwaka 2021, mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi ya pili ni Nigeria. Nigeria ni Taifa liko Afrika, lakini Nigeria ni namba mbili duniani kwa kupeleka tangawizi kwa wingi kwenye soko la dunia. Anapeleka asilimia 16.94 ni nchi ya Afrika hiyo. Nchi ya tatu ni Uchina.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi leo niongee kwa wivu, roho inaniuma. Ukiamuangalia Nigeria vizuri, naomba ndugu zangu mum-google vizuri, Nigeria analima tangawizi vizuri sana anapeleka kwenye mfuko wake wa Taifa, GDP anapeleka kutoka kwenye tangawizi anapeleka asilimia 23, siyo ndogo. Asilimia 23 kwenye GDP itoke kwenye tangawizi, siyo kidogo, ina maana Nigeria wanafanya kazi kwa bidii kuliangalia zao la tangawizi.

Mheshimiwa Spika, ukija ukimuangalia Nigeria huwezi kumtofautisha sana na sisi. Mimi nimeangalia kwa nini yeye anapeleka asilimia 23 kwenye GDP ya Taifa lake, ni kwamba Serikali imesimama imara sana kwenye kilimo cha tangawizi kwenye nchi ya Nigeria, imesimama imara kwa kuboresha miundombinu ya kilimo cha tangawizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi kwa nini naongea kwa wivu? Serikali ya Tanzania inashindwaje?

Mheshimiwa Spika, tangu mwaka 2000 niko humu ndani ninaongelea tangawizi, ninazungumzia tangawizi, ninazungumzia tangawizi. Serikali inasema hivi, inasema vile, naomba kipindi hiki, nazungumza kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu, lakini Waziri wa Kilimo asimame awajibu Watanzania wanaolima tangawizi kwa nini hili zao tunaliweka kama ni zao si kipaumbele?

Mheshimiwa Spika, nirudi tena niongee kwa uzito na ninyi mtani-support. Mwaka 2019 tulipata Covid 19, tangawizi ndiyo iliyotusaidia sana. Kila Daktari akisimama kuleni tangawizi, kila Dakrati akisimama tumieni tangawizi, lakini zao hili Serikali naomba nizungumze kwa uchungu, sikufurahi sana hakuna Waziri wa Kilimo, lakini hakuna hata Naibu Waziri wa Kilimo, anyway atasoma kwenye mitandao, kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kuliangalia hili zao vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa huu ni mwaka wa 22 nikisimama ni tangawizi mpaka wengine wananiita tangawizi, lakini it is fine. Naomba Serikali kipindi hiki izungumze inaiangaliaje tangawizi kwenye nchi hii?

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Same Mashariki wanaongoza kwa kile kilimo, lakini mioundombinu ya kilimo cha tangawizi Same Mashariki inaumiza roho. Wananchi wanatengeneza wenyewe hakuna wataalam, lakini bado wanaongoza kwa kulima kilimo hiki. Serikali iseme kwa nini haipeleki wataalam wa tangawizi, zile sehemu zinazolimwa tangawizi?

Mheshimiwa Spika, nimekwenda Madaba nikalima tangawizi eka 20, nimelima kule, miundombinu ni hivyohivyo kama Same Mashariki, hapana! Upande wa kilimo, Serikali nazungumza kwa malalamiko hamjawa serious. Upande wa zao hili la tangawizi wala hamlijali, lakini tulipopata Covid…

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mwanaisha Ulenge.

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nampa taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kwamba, anayoyazungumza ni sahihi kabisa, Serikali yetu siyo tu haijalipa kipaumbele zao la tangawizi, lakini haijatoa kipaumbele kwa mazao yote ya viungo nchini Tanzania ambayo yanaingiza fedha nyingi nchi za jirani. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Anne Kilango Malecela unapokea taarifa hiyo?

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, napokea na ninamshukuru sana Mheshimiwa.

Mheshimiwa Spika, wakati namalizia nikwambie ukweli kabisa Serikali isimame imara kuangalia haya mazao. Inachagua mazao kidogo inayafanyia kazi, haya ambayo inayapuuza kwenye nchi nyingine kama Nigeria yamepeleka asilimia 23 kwenye GDP ya nchi. Sasa ninajiuliza aah! kwani hawa wa-Nigeria wao wakoje, sisi tukoje?

Mheshimiwa Spika, ukiangalia hali ya hewa ya Jimbo la Kaduna kule Nigeria ndiyo hali ya hewa iliyopo Ruvuma, ndiyo hali ya hewa iliyopo Kilimanjaro. Serikali imechukua serious sana mazao ya viungo, lakini sisi tunayapuuza, hapana. Serikali katika hili mimi sitakubali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimejitahidi nilipoingia mwaka 2005 Jimbo la Same Mashariki, nilipoona wale wananchi wanalima sana tangawizi, nilianzisha ujenzi wa kile kiwanda. Naishukuru sana Serikali, nashukuru mbia aliyekuja kutuunga mkono kujenga kile kiwanda cha tangawizi pale Same Mashariki. Ukweli sasa tunagawana sisi pamoja na mshirika mwenzetu, lakini bado sasa hivi nazungumza tena nikiwa ninajivuna, Tanzania, Mamba Miamba tuna kiwanda cha kusindika tangawizi ambacho Afrika Mashariki hakipo, lakini Serikali inatusaidiaje? Tuna kiwanda, kilimo kiko wapi?

Mheshimiwa Spika, kile kiwanda ni kikubwa mno, kinahitaji tangawizi nyingi sana. Serikali isipokuwa imara kuboresha kilimo cha tangawizi hata kile kiwanda kitakuwa hakina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nasema ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hoja hii. Ningependa kuchangia hoja ya Kamati ya Miundombinu, nitachangia na hoja ya Kamati ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, ningeomba kuzungumzia na kuchangia kwenye zoezi la uhakiki wa line za simu, sasa hivi ulimwengu ni simu, simu ni kitu kidogo lakini simu sasa hivi ni kitu kipana sana. Hizi line za simu ni watu wa aina zote tunazo hizi simu, matapeli wana hizi simu, wezi wana hizi simu, wendawazimu wana hizi simu, wasomi wana hizi simu. Kwa hiyo, simu hii Serikali isipofanya uhakiki ikafahamu kweli line zake ziko na kina nani ni hasara sana katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, line ambazo zimesajiliwa na Serikali mpaka sasa ni zaidi ya line milioni 60 lakini mpaka tarehe 19, Januari zilizohakikiwa, Serikali ikafahamu haswa owners wa hizo line ni 58,432,669 ambayo ni sawa na 96.2% siyo mbaya. Lakini line ambazo hazijahakikiwa mpaka leo ni line 2,307,121 sawa na 3.8%, ni vyema na ni lazima kila mtu aliye na line ya simu kama kweli ni mtu ambaye ana ile line ya simu kwa upande ambao ni wa chanya ni lazima ahakikiwe. Sasa sisi kama Kamati ya Miundombinu tuliongea sana na Wizara tukaiomba iongeze muda wa hizi line kuhakikiwa na kweli niseme ukweli Wizara kila wakati tukiongea nao wamekuwa wanaitikia kweli. Sasa Serikali imeongeza mpaka tarehe 13 Februari, 2023. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nione tofauti kwamba mtu ambaye mpaka tarehe 13 Februari, 2023, line yake haijahakikiwa atakuwa yeye mwenyewe ana sababu zake binafsi kwa hiyo naunga mkono kwamba TCRA izime. Kwa sababu Wizara kila wakati imekuwa inaongeza muda na wamekuwa wasikivu sana Wizara ya Mheshimiwa Nnauye. Wamekuwa wasikivu sana ndani ya kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mwisho kabisa hii tarehe 13 Februari, 2023 mtu kama atakuwa hajahakiki line yake niseme kwamba yeye hiyo line yake alikuwa anaitumia labda kwa utapeli. Kwa hivyo, naunga mkono kwamba sasa tarehe 13 Februari, 2023, line zote tutasema, tutakubali kwamba zimehakikiwa, ambazo hazikuhakikiwa ni za wale ambao walikuwa wanatutapeli sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme ukweli line zimekuwa zinatumika vibaya mno mwenyewe niliyesimama hapa nikizungumza nimetapeliwa mara nyingi na akishakutapeli tu unastuka, ukimpigia humpati tena. Kwa hiyo, line hizi zilizokuwa zinatutapeli kiasi hiki sasa ni vyema zijue zimefika mwisho na baada ya taerehe 13, Serikali inasimama hao tunajua ni wale waliokuwa wanatutapeli ndiyo hawakuhakikiwa. Ninaunga mkono hoja kwamba Serikali ina haki ya kufunga baada ya tarehe 13. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja suala la Kamati ya Kilimo, suala la mbolea, naomba nizungumzie mbolea ya ruzuku. Hii mbolea ya ruzuku iliyotolewa kipindi hiki na Serikali, ambayo Serikali imelipa 50% ya ile mbolea, yaani kama mfuko wa mbolea ya urea ilikuwa ni shilingi 140,000, mwananchi anaununua ule mfuko kwa shilingi 70,000. Suala hili liliwafurahisha sana wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba kitu chochote, suala lolote linapokuwa kwenye introduction stage(mwanzo) kunakuwa na changamoto nyingi sana. Kipindi hiki hii mbolea ya ruzuku imekuwa na changamoto nyingi lakini nina uhakika Wizara imejifunza itakapofika kwenye stage ya growth, stage nyingine inayokuja mwaka huu tukifika wakati, nafikiri mwaka huu huko baadae, hawa watakuwa wamejifunza sana. Nikiri kwangu kuanzia Desemba 21 mpaka Januari 21, nilipata tani 212, tulipokea tani 212, nashukuru sana Serikali. Suala lililokera ambalo ni gumu na inabidi mabadiliko yatokee, vituo vya kupokelea ile mbolea. Kwangu mfano kwenye Jimbo langu ilikuwa ni makao makuu ya Jimbo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kabla ya yote naishukuru Serikali kwa sababu mbolea ilifika makao makuu ya jimbo lakini wananchi wanaoishi maeneo ya milimani, wananchi wanaoishi tarafa zingine ambazo siyo Tarafa ya Ndungu ilikuwa ni kazi lakini nilikuwa nawasihi wananchi kwamba kwa sababu Serikali ndipo inapoanza sasa kutoa ruzuku kubwa kiasi hiki, ninaomba mjikusanye mje kuchukua mbolea, nilikuwa kule kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tukiri kwamba hii ruzuku ni nzuri lakini ni lazima Serikali itafute njia ya kuwafanya wananchi wote kwenye maeneo mbolea ile ifike. Kwa sababu center zikiwa ziko mbali sana inakuwa kidogo ni tabu. Naomba niseme ninaunga mkono hoja hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Nakushukuru sana kwa kunifanya mchangiaji wa kwanza kwa hotuba hii muhimu sana ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kimaumbile nilivyoumbwa, siwezi kunyamaza. Nikitendewa jambo jema, nitasema, tena nitasema kwa sauti kali; lakini likitendwa jambo baya, nasema tena nasema kwa ukali zaidi. Sasa naomba nizungumze kwa sauti nzuri, sauti ya unyenyekevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, namshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mama Samia Suluhu Hassan. Nasema hivyo kwa sababu nimetumwa na wananchi walionichagua. Jimbo langu lilikuwa limejifunga, walioko milimani hawafiki tambarare, na walioko tambarare hawafiki mjini kwa sababu nilikuwa sina barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeanza kuongoza jimbo hili mwaka 2005. Miaka yote nilikuwa napewa pesa Shilingi milioni 350 na majedwali yote ninayo ya kuanzia mwaka 2005, Shilingi milioni 350 za kutengeneza barabara za TARURA. Tangu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameingia madarakani tarehe 19 mwezi wa Tatu mwaka 2021 mpaka leo, Jimbo la Same Mashariki limepewa fedha za kutengeneza barabara za TARURA Shilingi 5,200,000,000/=. Hili jambo siyo la kawaida. Wananchi wa Same Mashariki wanamshukuru sana Rais aliyeko madarakani, mpaka wananiuliza, hivi hizi pesa zilikuwa wapi miaka yote? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wangu asilimia 100 ni wakulima, na mkulima anahitaji barabara apeleke mazao yake kwenye masoko makubwa. Jimbo lilijifunga, walanguzi ndio wanaoweza kufika milimani kuchukua tangawizi kwa bei wanayoitaka wao; lakini sasa hivi wananchi wangu wanapeleka kwa magari, hawana wasiwasi, njaa jimboni kwangu imepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi tarehe 01/03/2023 walifanya sherehe kubwa kwangu ya kumshukuru Rais. Leo hii wamenituma kwa Waziri Mkuu, wameniambia tunakutuma kwa Waziri Mkuu na yeye ukamtume akamwambie Rais tunampenda sana, tunamshukuru sana, Mungu ambariki. Hapo nimesema kwa sababu nimefurahi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naingia jambo la pili. Serikali ya Chama cha Mapinduzi nawashukuru. Mimi natokea Mkoa wa Kilimanjaro. Mkoa wa Kilimanjaro elimu ilianza siku nyingi sana, shule zimeanza siku nyingi sana kwa sababu kuna waeneza dini, wamisionari walianza kuingia kwetu mwaka elfu moja mia nane themanini na kitu hivi. Walipoeneza dini wakajenga Shule. Baadae Serikali ikataifisha zile shule, ikajenga pamoja na wananchi. Hata hivyo, Shule zile zimechakaa sana, shule zile za msingi zimechoka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kuna waeneza dini, wamisionari walianza kuingia kwetu mwaka elfu moja mia nane themanini na hivi. Walipoeneza dini wakajenga Shule baadae Serikali ikataifisha zile Shule ikajenga pamoja na Wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule zile zimechakaa sana, Shule zile za msingi zimechoka sana, naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita. Nimeona na nimeletewa ripoti hapa ya pesa za boost za kwenda kuboresha na kujenga Shule za Msingi za Mkoa wa Kilimanjaro, nimepokea za kwangu, Charles angalia utaona za kwako huko. Kila Halmashauri ya Mkoa wa Kilimanjaro tunamshukuru Mungu tumepokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali naomba niwambie kitu kimoja Serikali ya Chama cha Mapinduzi, hizi Shule zitajengwa, hizi Shule zitaboreshwa, nitoe mfano; huu mwaka uliokwisha 2022 Serikali ilinipendelea iliniletea Milioni 100 za kujenga upya Shule ya Msingi inayoitwa Kihurio Kata ya Kihurio. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ile Shule ilijengwa, aliisimamia Mkurugenzi Vizuri sana na shule ile ikawa mpya. Madarasa tisa yalipokwisha sasa nakwenda kuona shule, Madawati! Ile shule iliyokuwa imechoka Madawati yalikuwa ni Magogo, yalikuwa ni madawati yaliyochoka, nimeshindwa kuingiza hayo magogo kwenye shule mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwenyewe kama Mbunge nimetengeneza madawati ya madarasa tisa kwa sababu nimeona niisaidie Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, imenipa Milioni 100 na mimi Mbunge niliyechaguliwa na wananchi nikafanya kidogo, nikafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiambie TAMISEMI, tumewashukuru mlivyotuletea hii pesa, tunaomba mpange vizuri mlete pesa za Madawati. Nina uhakika sio kwangu tu

kwa sababu ninaangalia mitandao ninaona ni sehemu nyingi sana. Sasa hilo limekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge mnisikilize kidogo, sasa naomba niongee na watanzania, naomba niongee kwa unyenyekevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nje watanzania wamekasirika sana lakini naomba niwambie watanzania kitu kimoja, Rais amechukizwa sana. Vilevile watanzania naomba niwambie jambo la tatu, Waheshimiwa Wabunge wote hapa ndani wamechukizwa waliposikia Rais akikabidhiwa ile ripoti ya CAG tarehe 29/3/2023 kila mtu alichukizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwambie Watanzania kitu kimoja, hizi shughuli kubwa kama hizi sisi Wabunge tunazifanya kwa utaratibu. Wananchi nje wanaona kama wabunge mbona hawasemi? Tunakwenda kwa utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu suala la CAG liko hapa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Suala la CAG sisi Wabunge tunakwenda nalo kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 Ibara ya 143(4) naomba uniruhusu kunukuu; “Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu atawasilisha kwa Rais kila taarifa atakayotoa kwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2) ya ibara hii. Baada ya kupokea taarifa hiyo, Rais atawaagiza watu wanaohusika wawasilishe taarifa hiyo kwenye kikao cha kwanza cha Bunge kitakachofanyika baada ya Rais kupokea taarifa hiyo na itabidi iwasilishwe katika kikao hicho kabla ya kupita siku 7 tangu siku ile kilipoanza kikao hicho kuketi. Iwapo Rais hatachukua hatua za kuwasilisha taarifa hiyo kwenye Bunge basi Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu atawasilisha taarifa hiyo kwa Spika wa Bunge au Naibu Spika ikiwa kiti cha Spika ki wazi wakati huo au ikiwa kwa sababu yoyote Spika hawezi kutekeleza shughuli za kazi yake ambaye atawasilisha taarifa hiyo kwenye Bunge” mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Spika wa Bunge anapokea taarifa ya CAG kesho, ikiwa na maana nataka kuwambia Watanzania taarifa hiyo haijaingia hapa Bungeni. Watanzania wajue kitu kimoja ambacho na sisi Wabunge tunakijua, Rais Samia Suluhu Hassan anahangaika mno kutafuta pesa kwa ajili ya maendeleo ya watanzania. Hawezi kukubali watu…

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni taarifa? Haya nakaa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba si tu kwamba hayajafika Bungeni lakini kwa mujibu wa Sheria ya Taifa ya Ukaguzi Kifungu cha 39(1) baada ya kuja Bungeni taarifa ya CAG ndiyo itakuwa public document na hata sisi Waheshimiwa Wabunge ndiyo tutaweza kuisoma in details taarifa yote na kila kitu kilichosemwa na CAG.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimeipokea na kijana ameidadavua ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lazima watanzania labda hawaelewi. Wakilalamika kwamba Wabunge hawasemi ni vema tuwambie kwamba tunafuata taratibu. Taratibu zitakpofika watanzania wawe na uhakika hakuna atakayepona. Rais hatakubali, Wabunge hatutakubali, sisi hatutakubali ambaye kweli tutakuwa tumehakikisha amechezea pesa za watanzania akaendelea kuzunguka kwenye nchi hii hapana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba na ninawaomba Watanzania kwa unyenyekevu waturuhusu sisi tunaowawakilisha tufuate utaratibu tusifanye kazi kinyume na utaratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo naomba kuunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kukushukuru kwa kunifanya kuwa mchangiaji wa kwanza. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa uhai, namshukuru Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali ya Chama Cha Mapinduzi Awamu ya Sita, nampongeza Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, anakwenda vizuri sana na wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wameleta salamu kwamba azipokee, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Bashe na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kuchangia, na leo ninaomba kuchangia kwa unyenyekevu mkubwa sana. Mheshimiwa Charles Kimei aliniuliza kwanini unachangia tangawizi kila siku, ninachangia tangawizi kila siku kwasababu kubwa moja, wananchi wangu wa Jimbo la Same Mashariki takribani asilimia 80 mpaka 85 wanalima zao la Tangawizi. Watanishangaa nikija nikaanza kuchangia kahawa, cocoa na miwa kwasababu wao wanalima zao la tangawizi, hivyo ni lazima nilizungumzie na kuisihi Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tulianza kulima Tangawizi mwaka 1988. Zao hili lililetwa na mzee mmoja anaitwa Mzee Kilango Chikila. Hatujui alilitoa wapi, lakini alilileta mwaka 1988. Tukaanza kulilima zao la tangawizi kwenye miinuko mikubwa ya mita 800 hadi 1500. Tangawizi iliyo bora ni ile inayolimwa kwenye miinuko mikubwa, na Jimbo la Same Mashariki ni jimbo la milima na milima hii ya tarafa mbili yote inalima tangawizi kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumelima tangawizi kwa miaka 34 sasa. Ninaongea kwa masikitiko kidogo lakini kwa unyenyekevu. Tumelima kwa miaka 34 sisi wenyewe bila kupata msaada kutoka Serikali Kuu; na kwa wakulima kama mnalima wenyewe bila ya kuboreshewa miundombinu ya kilimo ni lazima mtapata mazao hafifu. Tangu mwaka 2000 mimi nipo hapa Bungeni ninaongelea hili zao, lakini kwa uzito niliongea kuanzia mwaka 2005 nilipochaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninaiomba Serikali; na niongee kwa lugha ya unyenyekevu, lakini baadaye kama itapanda mnisamehe sana. Wananchi hawa wanalima hili zao wenyewe; nikiwa nina maana kwamba zao la tangawizi linatumia maji mengi sana, kwa hiyo tuna mirefeji lakini ile mifereji tumeitumia kwa miaka 34. Narudia tena, Serikali hatujapata msaada kutoka kwenu. Ni lazima Serikali mjue kwamba ninyi mnapaswa kuangalia miundombinu ya kilimo kwaajili ya wakulima. Hili ni hitaji la kikatiba la wananchi. Serikali ni lazima muwasaidie wakulima kwenye miundombinu ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka 34 hadi sasa ninapoongea tunategemea kulima tani 25,000 tu, lakini ujue tunavuna tani 25,000 tukiwa hatuna msaada wa Serikali. Iwapo Serikali mtafanya kazi yetu ya kikatiba ya kuboresha miundombinu ya kilimo ya Jimbo la Same Mashariki tunategemea tutavuna takribani tani 50,000. Juzi nilikwenda jimboni kufanya ziara nikaona nimletee Mheshimiwa Waziri picha hizi. Nikimaliza kuzungumza nitaomba hawa vijana waje wachukue wampelekee. Nimepiga picha miundombinu ya kilimo ya jimbo langu ambayo wananchi wanafanya wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa hii sio haki. Wananchi wanatengeneza miundombinu ya kilimo wenyewe ni kitu kigumu sana kwenye miinuko mikubwa ile ambayo Mheshimiwa Waziri wewe ulikuja, ulikuja kwenye ile miinuko. Na ninakuomba radhi, nitasema, pole sana kwa kuwa ulitapika sana kwenye ile miinuko. Ni kweli, yupo mwenyewe ameketi pale. Ile miinuko ni migumu lakini wananchi wale wanalima tangawizi kule, hawapati msaada wa Serikali, miundombinu ya kilimo yote hii wanatengeneza wenyewe. Mheshimiwa nitaomba upewe baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumeanza kuchakata tangawizi sisi. Tumepata kiwanda ambacho sisi wananchi wa kule tulikijenga wenyewe. Hata hivyo ninaomba niipongeze sana PSSSF kwasababu ilikuja kuwa mbia, na sasa tumejenga kiwanda cha tangawizi ambacho ni cha kwanza katika Afrika Mashariki. Tangawizi tunayovuna ni hii hapa, tangawizi tunayochakata ni hii hapa, tangawizi ya unga tunayotengeneza ni hii hapa.

(Hapa Mhe. Anne K. Malecela alionesha aina ya tangawizi zinazolimwa, zilivyochakatwa na zao la tangawizi katika mfumo wa unga)

MHE. ANNE K. MALECELA: Kwa sababu kile ni kiwanda hatuwezi kuchakata tangawizi bila TBS kuja. TBS wameangalia ubora wa tangawizi ya Same Mashariki. Mtaniwia radhi, mkiangalia vizuri mtaona ni tofauti na tangawizi nyingine zozote hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumze kitu kimoja, kwa siku moja ya masaa 24 kiwanda kile kinachakata tani 10, sijui mmenielewa! Tani 10. Sasa sisi wenyewe kwa mwaka tunalima tani 25,000, siyo tangawizi ya kutosha kwenye kile kiwanda. Sijui Serikali mmenielewa hapa? Kwa siku moja tunachakata tani 10, kwa mwaka mmoja tunavuna tani 25,000 ina maana kile kiwanda hakitapata tangawizi ya kutosha. Serikali ninaomba kwa unyenyekevu mkubwa nendeni mkaangalie miundombinu ya killimo na muiboreshe ili wananchi wale wavuna tangawizi kwa wingi, wawe na mazao ambayo yatakifanya kile kiwanda kipate malighafi ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwie radhi utakuwa. Angalieni Nigeria, Nigeria ina zao la tangawizi na ni zao la pili kuchangia kwenye GDP ya nchi asilimia 23. Kwa hiyo hili zao kama Serikali mtafanya kile mnachohitajika kufanya kwamba mkaboreshe miundombinu ya kilimo wananchi hawa watalima tangawizi kwa wingi. Mimi ninaomba hilo mliangalie vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema naongea kwa unyenyekevu lakini Mheshimiwa Bashe hapana niongee kwa ukali sasa hivi. Kwanini mnawafanyia wale wananchi hivi? Mnategemea wananchi walime wenyewe, wavune kidogo waishi vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Bashe sitaunga mkono hoja yako hata kidogo; na ninatangaza kuondoa shilingi mpaka utoe jibu ambalo litanifurahisha, ama sivyo leo hotuba yako ya kilimo itakuwa ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme ukweli; kwanini Nigeria wao wanavuna tangaziwi nyingi kiasi kile? Ni kwasababu Serikali ya Nigeria imesimama imara kwenda kushika wananchi wake wanaolima tangawizi, na ndiyo maana Tangawizi inakuwa mchangiaji wa pili wa GDP ya nchi ile kwa asilimia 23. Mimi naomba, nafikiri sina mengi ya kuzungumza, hoja yangu kubwa wewe kama Serikali uje Same Mashariki ukaisimamie miundombinu ya kilimo cha tangawizi. Bila ya hivyo mimi na wewe hatutaelewena, sitaunga mkono hoja nitangoja mwisho. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa jinsi ambavyo ametujalia amani kwenye nchi yetu ya Tanzania jamani, kwa sababu tuangalie hali halisi ya ulimwengu lakini Tanzania Mungu ametubariki mpaka leo nchi yetu imekaa vizuri. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuzungumza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Bashe na Mheshimiwa Naibu Waziri wake, tunakiri kwamba hawa ni Mawaziri vijana, wanafanya kazi vizuri na kikubwa ni wasikivu, wanapokea simu zetu, wanashirikiana na sisi, naomba niseme nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie dakika zangu nane vizuri. Kwanza naomba niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita kwa kujitofautisha. Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hassan imejitofautisha sana kiutendaji upande wa kilimo. Kwa nini nasema hivi? Tanzania nzima tuna Majimbo ya uchaguzi 264, katika Majimbo hayo, Tanzania Bara yako Majimbo 214, Tanzania Zanzibar yako Majimbo 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kidogo niongee upande wa Majimbo 214 ya Tanzania Bara. Haya Majimbo 214, Majimbo 188 ni Majimbo ya Vijijini na Majimbo ya Vijijini ni Majimbo ya wakulima. Kwa nini nilikuwa nasema Awamu ya Sita imejitofautisha. Rais Samia Suluhu Hassan amefanya kitu kikubwa sana kutuletea pesa za kutosha za barabara za TARURA. Tulipopata pesa za kutosha kwenye barabara za TARURA ina maana vijijini mazao yatatoka kwenda kwenye masoko makubwa kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme ukweli, mimi mazao yangu mengi yanatoka milimani. Tangawizi inatoka kwenye Tarafa mbili ambazo ni asilimia 70 ya Jimbo langu. Kule kulikuwa hakuna barabara. Walanguzi walikuwa wanafwata tangawizi milimani. Kwa hiyo wao walikuwa wanafaidi sana kilimo cha milimani pamoja na tambarare, lakini baada ya kupata pesa za kutosha za TARURA wananchi wangu sasa wanapeleka mazao yao kwenye masoko makubwa. Niipongeze sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Naona niishie hapo kwa hili la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije upande wa umwagiliaji. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana kwa kujali umwagiliaji kwenye Jimbo langu. Nitakushukuru halafu nitakuomba msaada. Mimi nina mazao mawili makubwa, tangawizi na mpunga. Tarafa mbili zinalima tangawizi, zinahitaji umwagiliaji. Nakushukuru sana Mheshimiwa Bashe, umeanza kuboresha umwagiliaji, umeanza na Kata mbili Kata ya Miamba na Kata ya Mpinji. Sasa naomba nikupe siri ambayo hujui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu Tarafa ya Mambavunda inategemea mto mkubwa unaitwa Mto wa Saseni ambako ndiyo mto huu unamwagilia tangawizi yote kule juu, lakini Mheshimiwa Waziri ule mto umeteremka ukaja mpaka Kihurio. Kihurio mto ule unalima mpunga, nikwambie ukweli ule mto sasa hivi umekwisha, umeharibika upande wa huku tambarare. Wananchi wa Kihurio wanalima mpunga, wananchi wa Kalemawe wanalima mpunga, ule Mto wa Saseni umebomoka lakini siyo wa kutengenezwa na Halmashauri ya Wilaya ya Same. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri, kwa sababu umeshakuja Jimboni kwangu usije wewe aje Mheshimiwa Mavunde, auone Mto wa Saseni ili aje akueleze muuboreshe Mto Saseni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme ukweli Kata ya Kihurio ndipo nilipozaliwa mimi. Sisi ni wakulima wa mpunga, tangu nimekuwa mtoto mdogo mpaka sasa bila ya Mto Saseni hakuna Kihurio, hakuna Kalemawe. Naomba Serikali mje muone mto muuboreshe Mto Saseni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia upande wa mbolea ya ruzuku. Nakiri Waheshimiwa mmeliongea hili lakini na mimi niongelee kwa upande wangu. Mheshimiwa nakushukuru sana, mbolea ya ruzuku nilikusumbua kwelikweli na hukuchoka kupokea simu zangu. Ulipokea simu zangu na ulinisaidia, lakini nikwambie ukweli; kwanza naipongeza Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan kutoa ruzuku asilimia 50 ni mara ya kwanza inatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inatokea mara ya kwanza mfuko unaonunuliwa kwa shilingi 140,000, mwananchi anaununua kwa shilingi 70,000. Tumpongeze Rais, amefanya kitu kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikiri kwamba kuanzia tarehe 21/12/2022 mpaka tarehe 21/1/2023, nikiri nilipokea mbolea ya ruzuku mifuko 4,240 ambazo ni tani 212. Mheshimiwa Waziri nikwambie ambacho wenzangu wamekwambia, hii mbolea yote ilikwenda Kata ya Ndungu. Kata ya Ndungu ni Tarafa ya Ndungu. Kwa hiyo, wananchi wa Tarafa za Milimani zote walikuwa wanakuja Kata ya Ndungu. Nashukuru, nakupongeza, umeanza vizuri, lakini changamoto ya kwamba haikufikia wananchi wengi ni kubwa sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, lakini hili mlisahihishe. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata muda, naomba leo niongee kwa kifupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kusema ukweli; hakuna awamu ambayo imejenga barabara katika nchi yetu kuzidi awamu ya sita. Hakuna mahali ambapo sasa hivi hapajengwi barabara. Ukienda mijini barabara zinajengwa, ukienda vijjijini TARURA wanafanya kazi ya kujenga barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nichukue nafasi ni kwa mara nyingine niishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya Awamu ya Sita, na niipongeze kwa kujenga barabara nchi nzima. Nimalizie kwa kusema kwamba Tanzania iko busy sana sasa hivi kwa miradi ya ujenzi wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, nirudi kwa Mheshimiwa Waziri Mbarawa. Hii Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, hii ni Wizara pana sana, ni Wizara ambayo ina shughuli nyingi sana. Amesema Mheshimiwa Mbunge jana pale, hii Wizara ina taasisi 22. Tuchukue taasisi moja tu ambayo nashukuru Waheshimiwa Wabunge mmiongea sana; taasisi ya TPA (bandari).

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari ni lango kuu la uchumi, na kweli kabisa; mimi niwapongeze Waheshimiwa Wabunge, mko very positive na kupata wawekezaji wa kusaidiana na Serikali upande wa bandari. Iwapo ile bandari tutaitumia vizuri, Serikali itaangalia vizuri na sisi Wabunge tukaridhia tunakwenda kukomboka, kukombolewa nchi yetu na Bandari ya Dar es salaam pamoja na bandari zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi huwa na-google sana na kuangalia, ukienda India tukubali Waheshimiwa Wabunge kwamba Wahindi ni wachumi wazuri; wenzetu India wametengeneza Wizara maalum ya bandari ambayo inaitwa Ministry of Ports Shipping and Water Ways. Wametengeneza Wizara maalum kwa ajili ya bandari kwa sababu wanajua uchumi uko kwenye bandari. Mimi nimesema tu sijasema zaidi ya hapo Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudi jimboni kwangu sasa. Mheshimiwa Waziri nakupongeza tena, nimesikiliza hotuba yako vizuri mno niende kwenye kifungu chako cha namba 106 ulipoongelea barabara yangu ya Mkomazi – Kisiwani – Same. Naomba nikushukuru, si mimi wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wamenituma, Mheshimiwa Waziri tunakushukuru sana, Waziri Mbarawa tunakushukuru sana. Tunakupongeza kwa sababu hii Serikali ya awamu ya sita imesikiliza kilio cha wananchi wa Jimbo la Same Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Same Mashariki silisemei kwa ukubwa, kwa ukorofi, tarafa mbili zote ziko milimani, narudia zinalima Tangawizi asilimia 72 ya tangawizi ya nchi nzima. Tarafa ya chini, Tarafa ya Ndungu inalima Mpunga, inalima inalisha Kilimanjaro inalisha Tanga. Lakini tulikuwa tunaponzwa na barabara ya Mkomazi – Kisiwani – Same Mheshimiwa Waziri tunakushukuru wananchi wamenituma nikushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fungu la 116 limeniambai kwamba barabara ya Mkomazi - Kisiwani - Same sasa imepata wakandarasi wawili na inajengwa kwa kiwango cha lami kilometa zote 97. Mkandarasi wa kwanza anaanza Same – Kisiwani – Mroyo kilometa 56.83 Mheshimiwa Waziri tunakushukuru sana, mkandarasi wa pili anaanzia Ndungu – Mkomazi kilometa 36. Mikataba hii itasainiwa mwezi wa sita, ambao ni mwezi ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie kabisa Mheshimiwa Waziri kwamba wananchi wameshona nguo, wanaume wameshona suti, wanawake wameshona vitenge; tutakuwepo kwa wingi sana mwezi wa sita utakapo kuja kwa ajili ya kusaini mikataba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi wananchi wa Same mashariki huu ni ukombozi mkubwa. Jimbo hili lilizaliwa mwaka 1995, Mbunge wa kwanza alikuwa ni Daniel Yona, alizungumza akiwa Waziri, huku akiwa Waziri alifanya kazi kuhusu barabara hii. Nikaingia mimi kwa kipindi cha miaka kumi kila wakati nazungumzia barabara hii. Akaingia mdada pale alipoingia naye akazungumza, na mimi nikaingia saa hiyohiyo nikawa Mbunge wa kuteuliwa nikasimama imara nikizungumzia barabara hii, nimerudi sasa nazungumzia barabara hii; lakini awamu ya sita tunaishukuru imetusikia imetupa barabara hii, ahsante sana, ninaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nazungumza kwa uchungu sana kuhusu Dar es salaam. Nazungumza kwa uchungu kuhusu Dar es salaam na ninaomba Serikali mnisikilize vizuri. Dar es salaam yalikuwa ndiyo makao makuu ya nchi yetu tangu tumeitwa nchi. Awamu ya tano ndiyo imekuwenda kufanya kimatendo kuhamisha makao makuu kutoka Dar es salaam kuja Dodoma tunashukuru sana. Lakini, Dar es salaam inajengwa barabara nzuri, lakini Dar es salaam inatatizo kubwa mvua zinaponyesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali inisikilize, siitumi, inisikilize. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aandike historia, aandike historia ya kuitoa Dar es salaam kwenye matatizo ya maji wakati wa mvua. Kwa nini nasema hivyo? Sisi tuna ma- engineer wengi sana. Ukienda TANROADS yenyewe ina ma- engineer 306 walioko kwenye ajira za kudumu. TANROADS hiyo ina Ma-engineer 238 walioko kwenye ajira za mikataba. Hivi wananshindwaje hawa Ma-engineer kukaa chini wakatumia Elimu yao wakaondoa lile tatizo lililopo Mkoa wa Dar es salaam?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Dodoma ni makao makuu, lakini hata kama Dodoma ni makao makuu, Dar es salaam itaendelea kuwa mji mkuu wa kibiashara na Tanzania tukubaliane kwamba Dar es salaam bado itaendelea kuwa ni jiji ambalo linavuta watu na linapendeza mpaka mwisho wa maisha ya kuishi huku duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naiomba Serikali kipindi hiki cha Mama Samia Suluhu Hassan asimalize kipindi chake hiki cha kwanza kabla hajatatua tatizo la maji yanayotuama, yanayojaa na kukosa njia kiasi kwamba wananchi wanashindwa kuendesha magari mimi juzi alipokuja Makamu wa Rais nilishtuka nikasema atashindwa kupita akitoka airport.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona nimegongewa kengele lakini naiomba Serikali itumie Ma-engineer wote tulionao kipindi hiki hiki cha Mama Samia cha kwanza iondoe matatizo ya Mkoa wa Dar es Salaam. Ma-engineer tumieni elimu yenu Mheshimiwa Mbarawa una ma-engineer wengi kaeni muangalie hili tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya. Tunapowapongeza Waziri na Naibu Waziri kweli wanafanya kazi sana siyo kwamba tunawatania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami naongea suala hilo hilo la tembo. Jimboni kwangu wananchi hawana raha, wananchi hawana furaha, matatizo ya tembo kwenye Jimbo la Same Mashariki naomba tafadhali haya makabrasha mawili haya yaje mbele yako apelekewe Mheshimiwa Waziri, kwa sababu gani? Kama miaka mitatu hivi madhara yaliyofika mashambani kwa wananchi wangu, mpunga, mahindi, miaka mitatu, takribani miaka mitatu hata hicho mnachokiita kifuta jasho wananchi hawajapewa, sasa nianze upande wa vifo.

Mheshimiwa Spika, kabrasha hili linazungumzia vifo. Naanzia Muheza, Kenneth Edward Mazengo - Muheza, huyu alijeruhiwa tangu tarehe 24 Julai, 2022, wala Serikali haijamuangalia. Rayson Eminiel Mjema wa Kijiji cha Muheza alijeruhiwa na tembo tangu tarehe 26 Januari 2022, wala Serikali hamjampa hata senti tano. Ally Mhina Mbogo Makokane aliuawa tarehe 9 Julai, 2022 na tembo lakini Mheshimiwa Waziri mambo makubwa kama haya Serikali hamjawaona wananchi, na Zuhura Mapande wa Kijiji cha Muheza aliuawa tangu tarehe 17 Agosti, 2022 aliuawa na tembo.

Mheshimiwa Spika, nilikuwepo mwenyewe Jimboni niliona aibu kwenda kumuona yule mama alivyochanwachanwa na tembo lakini Serikali hamjaona watu kama hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili kabrasha lote nililoshika mkononi hapa ni mazao ya wananchi wa Jimbo la Same Mashariki. Mimi ninahisi Mheshimiwa Waziri nisikilize vizuri, hawa tembo wangekuwa kule ndani ya National Parks wana maji ya kutosha, wasingekuja kwa wananchi huku, wangekuwa wana chakula cha kutosha wasingezunguka na kula mpaka wali uliopikwa na wananchi, angalieni vizuri ndani ya National Parks kuna hali gani?

Mheshimiwa Spika, naomba nikwambie. Naanza upande wa uharibifu wa mazao ya wananchi. Twende Kata ya Maore Kijiji cha Maore tembo wameharibu ekari 74.5 hapa ni kaya 67 zote wananchi hawakuvuna kitu, njaa. Kata hiyo hiyo ya Maore nenda Kijiji cha Mpirani ekari 21 mpunga na mahindi hapa ni kaya 21 wananchi hawakuvuna kitu. Kata hiyo hiyo ya Maore Kijiji cha Mheza kaya 367 ekari takribani 512, ekari zote hizi wananchi hawakuvuna kitu. Kijiji cha Kadando takribani kaya 54 ekeri 66, wananchi hawakuvuna kitu, tembo.

Mheshimiwa Spika, twende Kata ya Kalemawe, Kijiji cha Kalemawe kaya tisa na ekari tisa za mahindi wananchi hawakuvuna kitu. Twende Kijiji cha Makokane kaya 132, ekari 143 za mpunga na mahindi wananchi hawakuvuna hata hindi moja. Kijiji cha Karamba kaya 30, ekeri 31 mahindi, maharage, mboga za majani hawakuvuna kitu wananchi. Kata ya Nungu Kijiji cha Misufini kaya 95 ekari 145 wananchi hawakuvuna kitu. Kijiji cha Nungu kaya 33 ekari takribani 35 hawakuvuna kitu.

Mheshimiwa Spika, nikianza Kijiji kwa Kijiji kwangu ni taabu. Jimbo la Same Mashariki ni shida, nakuomba Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja miaka miwili iliyopita, kote huku nilimpeleka hakuna kitu kimefanyika mpaka leo. Juzi nasikia Diwani anaiambia Mheshimiwa Waziri ametuma watu wake wamekuja kuona mahali pa kujenga Kituo cha Askari mimi wala hilo silipokei, wamekwenda kuona je, wamejenga? Huko ni kuona wananchi wangu wanakufa kila siku, wananchi wangu hawana mazao, hawana chakula, wana njaa, tembo.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, mimi sitaunga mkono hoja, naomba Mheshimiwa Waziri anijibu anawafanyia nini wananchi wangu kuhusu tatizo la tembo. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru sana, lakini nikiri kwamba una Wabunge wazuri sana, tangu asubuhi saa 3:00 mpaka saa hizi nafikiri asilimia kubwa ya Watanzania wameelewa azimio lako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niseme ukweli, nitazungumza kidogo wala sitachukua muda wangu mrefu. Ni kweli nimemsikiliza mtoa hoja Mheshimiwa Waziri, nimemsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu wamezungumza jambo kubwa, lakini mimi nafikiri nitaliongeza kidogo kwamba huu sio mkataba, huu sio mkataba wa kiutendaji.

Mheshimiwa Spika, haya ni makubaliano kati ya nchi na nchi. Tumepata Uhuru mwaka 1961 Waheshimiwa Wabunge, nina uhakika Serikali zote zote zimeingia makubaliano kama haya, ni kwa sababu tu tulikuwa hatuletewi hapa kuridhia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano, Serikali ilishawahi kuingia makubaliano na nchi ya Marekani kama haya haya upande wa afya; Serikali ilishawahi kuingia makubaliano kama haya na Canada upande wa elimu, hakuna kitu kipya Waheshimiwa Watanzania; na Serikali ilishawahi kuingia makubaliano kama haya na China upande wa biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Watanzania wanachanganywa, lakini hili jambo la makubaliano ni jambo la kawaida kabisa na ninaomba Watanzania muone kwamba kipindi hiki linaleta hekaheka kwa sababu imepitishwa hapa turidhie. Hii ni mara ya pili tunaridhia.

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Issa Mtemvu.

TAARIFA

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, mchangiaji anachangia vizuri sana, eneo la historia kwa makubaliano kama hayo unayoyasema, hata juzi tu tunayo makubaliano kama haya ya bomba la mafuta kutoka Uganda hadi Ohima, Tanga. Kwa hiyo, ni makubaliano yanayofanana kabisa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, naipokea Taarifa hiyo na tena ninakumbuka vizuri tuliridhia.

Kwa hiyo, Waheshimiwa Watanzania wetu, wapiga kura wetu msichanganywe, hakuna kitu kipya hapa. Hapa kitu kinachosumbua watu Awamu ya Sita inakwenda kushika nchi tena, hakuna kitu kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge Serikali ya Chama cha Mapinduzi sio wajinga, wanaingia uchaguzi mwaka ujao, wana uchaguzi mwaka 2025, walete bomu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawawezi kuleta bomu, hiki kitu ni kitu kinakwenda kutuimarisha, na Waheshimiwa Wabunge mkakitumie vizuri mtakapoomba kura. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongee jambo la pili; mimi nimewafurahia Watanzania sana, nimewapenda Watanzania sana kwa sababu Watanzania wameonesha hofu yao, wameonesha hofu yao kubwa, wakamfanya na Rais amefurahi sana, wameifanya na Serikali imejua Watanzania wanataka nini. Kama mmegundua, mimi nimewasikiliza kwa siku zote nikitika nikirudi nyumbani nawasikiliza kwenye njia nyingi, Watanzania wanaipenda nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania wanafahamu kama bandari ndio lango kubwa la mapato ya nchi yao. Kwa hiyo, wameona aah, bora tuseme, mimi ambao nawaweka kando ni wale wapotoshaji wale siwasifu, lakini Watanzania nimewapenda mno, mlitumia haki yenu ya Kikatiba, mmezungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Watanzania kilichowasumbua ni hofu; ahh hii bandari yetu, hiyo mikataba itakayoingiwa itakuwa mikataba mibovu, itamaliza nchi yetu, ndio kimewasumbua Watanzania, lakini naomba niwatoe hofu Watanzania kwa kitu kimoja kikubwa.
Mheshimiwa Spika, mimi nimetulia kwenye mitandao nikasema hivi Rais hajasema kitu chochote kuhusu mikataba?

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu nimnukuu Mheshimiwa Rais. Naomba nimnukuu Mheshimiwa Rais na kwa sababu yeye anazungumza kwa sauti ndogo na mimi nizungumze kwa sauti ndogo kidogo.

Mheshimiwa Spika, nimemsikiliza Mheshimiwa Rais jana ITV wamemleta kwenye kipindi cha mubashara, Rais anasema hivi; “Jamani mikataba hii ina aina zake, unajua kabisa mkataba wa aina hii hauwezi kuwa na vifungu hivi vikawa ndani ya huo mkataba, lakini unaukuta mkataba wa aina hiyo na kuna kifungu cha ajabu ajabu kimo ndani ya huo mkataba ambacho hakipaswi kuwa ndani ya huo mkataba, lakini umepita kote, njia zote na mkataba ukaenda ukafanya kazi na sasa waliofanya wanadai ni kimkataba, ni kimkataba, kwenye mkataba ipo. Sasa unawapa watu wengine, hebu someni huu mkataba, wanasema huo mkataba mama haukupaswa kuwa na vifungu hivi. Sasa unawauliza ilikuwaje vikaingia? Wanaangaliana machoni. Dhambi zetu sisi wenyewe, sisi wenyewe tunauwa nchi yetu, sisi wenyewe. Unaruhusu vifungu vya ajabu vinaingia kwenye mikataba isiyopaswa, kwa hiyo, huku kwenye mikataba kuangalieni vizuri,” mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rais ameshawaonesha Watanzania kwamba hataki mikataba mibovu, alilizungumza hili kabla hatujafikia kujadili hili azimio hapa. Naomba Watanzania wawe na uhakika kwamba huyu siye, hatakubali mikataba mibovu. Wawe na uhakika kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi, inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inakwenda kuleta ufanisi ndani ya bandari zetu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja na n awaomba na Waheshimiwa Wabunge tusimameni imara tuipe nafasi Serikali ifanye kazi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kusema kwamba naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi tangu tumepata uhuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi imekuwa inafanya jitihada kubwa sana kujenga barabara, lakini leo naomba hotuba yangu niongee barabara kwa Tanzania, nije niongee barabara kwa Afrika Mashariki, mwishoni nitamalizia kwa Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nienze kwa kutoa pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais ambaye ni Rais wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwamba tarehe 25 Mei, 2022 atapata tuzo ambayo niseme ukweli tuzo hiyo Mheshimiwa Rais anaistahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini naona kwamba tuzo anaistahili Mheshimiwa Rais; basi nianze kwa barabara mtandao wa Tanzania. Tanzania ina mtandao wa barabara wenye urefu wa takribani kilometa 180,792 kati ya kilometa hizo kilometa 144,429 zipo chini ya TAMISEMI ambazo zinajengwa na TARURA kilometa 36,361.95 zipo chini ya Wizara ya Ujenzi zikijengwa na TANROADS. Kilometa 11,512.9 ni barabara za lami hii ni sawa na asilimia 32 na zilizobaki ni barabara za changarawe.

Mheshimiwa Spika, sasa nije kwenye Afrika Mashariki ambapo Waheshimiwa Wabunge naomba mnisikilize vizuri. Tanzania ina mtandao wa barabara wa kilometa 36,362; za lami ni kilometa 11,513 za changarawe ni kilometa 24,549; asilimia 32 ya barabara zetu ndio zina lami, hiyo Tanzania.

Mheshimiwa Spika, twende Kenya, Kenya ina kilometa 21,583 kwa ujumla; za lami 12,220 zilizobaki kilometa 9,363 lakini Kenya ina asilimia 56 ya barabara zenye lami, lakini mtandao wake ni kilometa 21,583; Tanzania ni kilometa 36,362. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende Uganda, Uganda ina mtandao wa kilometa nchi nzima 21,000; kilometa 5,300 ndio zenye lami; kilometa 15,600 ni za changarawe.

Mheshimiwa Spika, twende Rwanda, Rwanda ina mtandao wa barabara kilometa 14,000; kilometa 2,662 ndio za lami. Twende Burundi, Burundi ina mtandao wa barabara kilometa 12,000 zenye lami ni kilometa 1,647.

Mheshimiwa Spika, Watanzania tunajiona kama sisi tupo nyuma, sivyo, sio hata kidogo, Tanzania inakwenda vizuri sana kwenye ujenzi wa barabara na niwaambie ukweli kama Kenya ingekuwa na mtandao mkubwa kama wa kwetu ingekuwa imetuzidi kwa asilimia 3.1; lakini Watanzania tunajiona kama nchi yetu haipo vizuri kibarabara, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania katika Afrika Mashariki tunafanya kazi nzuri sana naomba Mheshimiwa Waziri pamoja na TANROADS kwa ujumla pamoja na TARURA nitoe pongezi kubwa sana katika ujenzi wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa turudi Dar es Salaam, mimi nitaongea kwa muda mfupi, katika kipindi cha miaka sita Wizara ya Ujenzi kupitia TANROADS wamelijenga Jiji la Dar es Salaam vizuri sana, naomba nitoe pongezi kubwa sana miaka sita iliyopita ulikuwa unaona Nairobi ndio jiji katika Afrika Mashariki, hapana, sasa hivi jiji la Dar es Salaam ni jiji la kimataifa kwa sababu ya ujenzi wa barabara unaofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kweli Mheshimiwa Rais anakwenda kupata tuzo aliyoistahili, kaangalieni Dar es Salaam sasa hivi, nirudi kwenye takwimu Dar es Salaam ina ukubwa wa kilometa 655.6 zenye lami na gharama za barabara za Dar es Salaam ni trilioni 2.055. Naomba niipongeze sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mbarawa, naomba niwapongeze TANROADS na TARURA kuifanya nchi yetu iwe na barabara bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Watanzania muwe mnaangalia takwimu, wale mnaoweza ku-google m-google vizuri bado Tanzania katika Afrika Mashariki tupo vizuri sana upande wa barabara. Situtaka kuongea kwa dakika nyingi nilitaka kuitoa hiyo picha kamili ya nchi yetu upande wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nakupongeza sana Mheshimiwa Mbarawa. (Makofi)