Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hussein Nassor Amar (36 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kuweza kusimama mahali hapa kwa siku ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ndiyo mara yangu ya kwanza kusimama kwenye Bunge hili la Kumi na Moja, napenda kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale kwa kunipa kura nyingi sana za kishindo mimi pamoja na Waheshimiwa Madiwani. Kwa kipindi cha pili Halmashauri yetu iko ndani ya mikono ya CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa Mpango wake mzuri ambao ameuweka hapa mezani. Pia napenda niseme jambo moja ambalo lilizungumzwa jana, upande wa upinzani walisema Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwenye kampeni zake alipiga push-up.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema kwamba zile zilikuwa ni mbinu, lakini hata ninyi kuna mizunguko mlikuwa mkiifanya, ile zungusha pamoja na helicopter nyingi kwenye Jimbo langu mara nne, lakini hamkufua dafu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kujielekeza kwa kuipongeza hotuba hii nzuri. Na mimi pia naungana na wenzangu kuhusu ujenzi wa reli. Ujenzi wa reli utaongeza mapato makubwa sana katika nchi yetu, lakini pia sisi wananchi tunaoishi pembezoni mwa nchi ni kwamba vifaa mbalimbali vitashuka bei.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano, cement kwa Kanda ya Ziwa ni shilingi 18,000/=, shilingi 20,000/= mpaka shilingi 22,000/=; wakati Iringa Mheshimiwa aliyekuja kuwekeza nchini kwetu, Mheshimiwa Dangote, amesema kwamba cement itashuka bei mpaka shilingi 8,000/=. Kwa kupitisha kwa njia ya barabara, tutaendelea kuipata ile cement wananchi wa Mwanza na Kanda ya Ziwa kwa ujumla kwa bei kubwa. Lakini pindi reli ile itaanza kufanya kazi, naamini kabisa kwamba cement na mazao mbalimbali kwa kuja Dar es Salaam na mali mbalimbali kutoka na kwenda Kanda ya Ziwa, zitashuka bei.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu ni mzuri, lakini kuna jambo moja naomba nishauri, kuna bwana mmoja na jeshi kubwa sana, hakuingizwa kwenye Mpango huu, naye anaitwa mzee watoto wa mitaani. Mpango huu haukuwekwa. Kwa nini? Kwa sababu jeshi hilo kila mwaka linaongezeka. Serikali ina mpango gani kupunguza watoto wa mitaani? Mtaa hauzai! Serikali ina mpango gani kuhusiana na suala hilo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale, mimi nimekuwa Mbunge wao takriban huu ni mwaka wa sita, nimekuwa nikipigania tatizo kubwa la maji. Mkondo wa Ziwa Victoria unaanzia kwenye Jimbo la Nyang’hwale, lakini cha ajabu wananchi wa Nyanghwale hawana maji.
Mwaka 2013, Waziri Maghembe nilikataa kupitisha bajeti yake; bahati nzuri Serikali kupitia Benki ya Dunia tuliweza kupewa mradi huo wenye thamani ya fedha shilingi bilioni 15.7. Cha ajabu, mpaka leo hii pesa ambayo imetoka ni shilingi bilioni 1.8. Bajeti ya mwaka 2015/2016 tuliongezewa shilingi milioni 752 lakini fedha hiyo haijatoka. Sasa hivi Wakandarasi wamesimama, hawaendelei na kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, kwa mwaka wangu wa sita waje wamejipanga vizuri Wizara ya Maji. Sitakubaliana! Sisi wananchi wa Nyang’hwale tuna mkosi gani? Naiomba Serikali ya Chama cha Mapinduzi, ni Serikali sikivu.
Ndugu zangu, naomba nizungumzie suala la elimu bure. Naishukuru Serikali, imeanza kutekeleza; lakini kuna jambo moja sikuliona ndani ya Mpango kuhusu elimu. Kuna familia nyingine, kaya moja unaikuta inajaza darasa; lakini kuna kaya moja ina watoto wawili. Je, ndani ya Mpango huu, kaya moja ina watoto inajaza darasa moja, kaya mbili zinajaza madarasa mawili.
Ndugu zangu, tujaribuni kuliangalia; ndani ya Mpango tuwekeeni utaratibu mzuri. Yule ambaye ana watoto kuanzia 10, 20, au 30, awekewe naye Mpango mzuri. Nusu ichangie Serikali na nusu achangie. Hili suala ni la msingi sana. Kuna wengine wana wanawake kumi, wengine watano na wengine wamejaliwa kuzaa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alifanya ziara kwenye jimbo langu. Alikuja akaahidi Kituo cha Afya Kalumwa, kukipandisha kuwa Hospitali ya Wilayana tayari imeshapandishwa, lakini ukifika pale, hali ni mbaya! Kuna wodi ya akina baba ina vitanda nane. Wagonjwa wa aina zote wanalazwa mle. Naiomba bajeti hii inayokuja, Wizara ya Afya mje mmejipanga vizuri kwa ajili ya kuboresha hospitali yetu ya Wilaya ya Nyang’hwale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miundombinu, kwa kweli miundombinu ya Wilaya ya Nyang’hwale, kuna barabara moja ambayo imeahidiwa kuanzia mwaka 2010 alipokuja Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, alituahidi kutujengea barabara kutoka Busisi kupita Busorwa, kupita Karumwa, Nyang’hwale kupita Msala kwenda Kahama. Leo miaka mitano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alikuja tena mwaka 2011 wakiwa katika msafara huo, Mheshimiwa Waziri Maghembe alikuwa yumo, Mheshimiwa Majaliwa alikuwa yumo, Mheshimiwa Rais wetu huyu wa sasa hivi wa Awamu ya Tano alikuwa Waziri wa Ujenzi na Mheshimiwa Jakaya Kikwete, walisimama na wakalizungumzia suala la barabara tutajengewa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia kwenye Mpango huu, barabara hii haimo. Naomba sasa hii awamu ya hapa kazi tu, atutekelezee. Anaielewa vizuri hiyo barabara, alituahidi akiwa Waziri na leo ni Rais wa nchi. Ninaomba ahadi ya Rais, iwekeni humo barabara hiyo kwenye Mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kilimo. Wananchi wa Nyang’hwale tuna mabonde mazuri sana, tuna mito mingi, maji yale yanaporomoka yanakwenda Ziwani. Naomba tuweke mpango mzuri wa kuyatega yale maji yaweze kuwasaidia wakulima wetu. Tuweze kupata maji kwa mifugo na matumizi ya binadamu, pia tuweke mpango mzuri wa kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema tunataka tunyanyue viwanda vidogo vidogo, vya kati na vikubwa: Je, material hayo yatapatikana vipi? Sisi wananchi wa Nyang’hwale ni wakulima wa mpunga, tunategemea mvua za masika, lakini kama tutatengenezewa mabwawa mazuri, kwa umwagiliaji tutalima mara mbili au tatu na tutakuwa watu wazuri sana wa kuweza kuongeza kipato chetu kwa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya njema kwa siku ya leo na kuweza kusimama hapa. Pia nimshukuru Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa na Baraza lote la Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kutumbua majipu. Ni kazi nzuri sana inayofanyika pamoja na kwamba wengine wanakasirika lakini ndiyo ilikuwa kiu ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kuunga mkono hotuba hii nzuri ambayo imesheheni mambo mazuri. Napenda niwakumbushe wenzetu Kambi ya Upinzani, kuna mchangiaji mmoja alisema kipindi cha nyuma kwamba ninyi wana CCM mnapenda sana kupongeza, mimi sipongezi, wakati Mwenyezi Mungu anasema usiposhukuru kidogo hata kikubwa hauwezi ukashukuru. Hata kwenye maombi kwanza unamshukuru Mwenyezi Mungu kwa alichokupa na unachohitaji unaendelea kuomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo, napenda niikumbushe Serikali yangu Tukufu, tunaambiwa tunalalamika, hatulalamiki tunakumbushana. Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni kwenye Jimbo langu la Nyang’hwale tulimweleza matatizo yetu na akaahidi. Tulikuwa na ahadi ambayo tuliahidiwa na Rais wa Awamu ya Nne kuhusu barabara ya kutoka Kahama – Nyang’hwale - Busolwa - Busisi kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami. Pia alipokuja Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wakati wa kampeni nilimkumbushia hilo na akaahidi kwamba barabara hiyo itajengwa. Kwa hiyo, naendelea kukumbusha barababa hiyo ijengwe angalau kwa kilometa chache kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda niishukuru Serikali yangu kwa ahadi yake ya kusambaza umeme vijijini. Jimbo la Nyang’hwale tayari tumeshapata umeme lakini ni kwa kiwango kidogo sana. Vijiji vingi havina umeme na Watanzania wengi waliopo Jimbo la Nyang’hwale wanasuburi kwa hamu umeme kwa ajili ya kufanya kazi zao mbalimbali ambazo zinahitaji umeme. Wanahitaji wafunge mashine ndogondogo kwa ajili ya kukamua alizeti, mpunga na mambo mengine.
Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Nishati muda utapofika utukumbuke sana Jimbo la Nyang’hwale kutukamilishia ahadi ambazo ametuahidi mara nyingi kutupa umeme katka Jimbo la Nyang’hwale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Jimbo langu la Nyang’hwale tuna tatizo kubwa la maji, nimeshaongea tangu nilivyoingia mwaka 2010. Nimezungumzia suala la maji kwa nguvu zote na Serikali ilisikia na ikaitikia wakatuahidi kutujengea mradi wa maji. Tuliahidiwa mradi mzuri na mkubwa wa kutoka Ziwa Victoria na kusambaza maji katika Jimbo la Nyang’hwale. Tumepangiwa shilingi milioni 15.7 ndani ya miaka mitano na huu wa sita tumeshapewa shilingi bilioni 1.9. Naomba sasa ili niweze kurudi tena Bungeni mwaka 2020 mradi huo wa maji ukamilike.
Mheshimiwa Waziri Mkuu kama utapenda tuwe pamoja tena mwaka 2020, naomba mradi huu ukamilike. Waziri wa Maji nipe hayo maji ili mama zangu na dada zangu waweze kunipa kura tena niwe na jambo la kusemea vinginevyo sirudi tena. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la afya. Kwenye Jimbo langu kuna hospitali ambayo imepandishwa hadhi na kuwa Hospitali ya Wilaya lakini kwa bahati mbaya hospitali ile ina majengo ya kizamani, haina wodi, haina x-ray na vifaa tiba hakuna. Kuna wodi mbili tu, wodi moja ya akina baba wanachanganywa wagonjwa wa maradhi yote mle ndani na wodi ile ina vitanda kama tisa tu. Kwa hiyo, naomba ili sasa iwe Hospitali ya Wilaya tuletewe vifaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na vifaa tiba na kupanua majengo ikiwemo majengo ya wodi ya kulaza wagonjwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipokuja Jimboni kwangu aliwaahidi wachimbaji wa madini ya dhahabu kwamba watatengewa eneo, kuna eneo moja linaloitwa Mwasabuka huko Nyijundu, alisema watagawiwa wachimbaji wadogo wawe huru wapewe leseni ili waweze kuchimba na waweze kusaidiwa na Serikali ili waweze kunyanyua kipato chao na kipato cha Serikali.
Naomba kumkumbusha Waziri wa Nishati na Madini kwamba ahadi hiyo aifuatilie ili wananchi hawa, vijana hawa ambao wanapata kipato chao kutokana na uchimbaji wa madini basi wawafikirie na kuweza kuwatekelezea ambayo waliwaahidi wakati wa kampeni wasione kwamba tulikuwa tunawadanyanga kwa ajili ya kutupa kura, waone kabisa tulikuwa tukiwaahidi mambo yaliyo sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu, naishukuru Serikali imeanza kutekeleza mpango wa elimu bure. Kama walivyosema wachangiaji wengine, tuangalie stahiki za walimu wetu, wazipate kwa muda ili wawe na ari na kasi na nguvu mpya kabisa ya kuweza kusimamia suala la elimu. Kwa sababu stahiki zao zinachelewa, zikichelewa amani ama imani ya kazi inashuka. Kwa hiyo, naiomba Serikali ijaribu kuangalia sana stahiki zao ili waweze kuwa na moyo wa kufanya kazi hiyo bila kutetereka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda kuongelea kuhusu wafugaji. Katika Jimbo la Nyang’hwale wafugaji wetu wamesahaulika. Nimeangalia katika mipango yote iliyopita sijaona wafugaji wa Jimbo la Nyang’hwale wamefikiriwa nini, hakuna soko, malambo wala majosho. Kwa hiyo, naomba wafugaji wa Jimbo la Nyang’hwale nao wafikiriwe kuboreshewa soko la mazao ya mifugo yao. Nimeangalia kwenye kitabu cha mpango, Mkoa wa Simiyu vinajengwa viwanda vitatu vya ngozi lakini Geita hakuna kiwanda hata kimoja cha ngozi, inakuwaje namna hii? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa Jimbo la Nyang’hwale na wakulima wote wa Tanzania kwa kweli wamekuwa wanakata tamaa kutegemea kilimo kwa sababu soko la mazao siyo la uhakika, pembejeo zinakuja mbovu, za gharama kubwa na zinachelewa kufika. Naiomba Serikali, kwa sababu wimbo mkubwa ni kwamba tuwasaidie wakulima, hebu tujaribu kweli kuwasaidia wakulima kwa kuwasaidia pembejeo na soko lao liwe la uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kusahau napenda nimkumbushe Mheshimiwa Waziri Mkuu, kulikuwa na mchakato wa Makao Makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale na bahati nzuri ulishaisha na Serikali ikatamka Makao Makuu ya Nyang’hwale yatakuwa Karumwa. Kwa bahati mbaya mpaka sasa hivi hati ya kujulisha kwamba Makao Makuu ya Nyang’hwale yako wapi haijatoka.
Mheshimiwa Waziri Mkuu utakaposimama hapa, waambie wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale, hawa wapinzani hususan CHADEMA niliowashinda vibaya sana wanapiga kelele na kusema kwamba haya Makao Makuu hayapo mnadanganywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Naomba utakaposimama uwajibu hawa Watanzania wa Nyang’hwale pamoja na hao wapinzani, waelewe Makao Makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale yako Karumwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia kuhusu ardhi. Tuna ardhi nzuri, tunaomba ipimwe ili wananchi wetu waweze kunufaika na ardhi yao. Kwa bahati mbaya kuna zile hati za kimila, wananchi wetu wamepimiwa tangu mwaka 2011 mpaka leo hawajazipewa, ni zaidi ya hati 800 na kitu. Serikali ina mpango gani sasa kuwapa hizo hati za kimila ili ziweze kuwasaidia hawa wananchi kupata mikopo midogo midogo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo napenda kulizungumzia ni UKIMWI. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI na dawa za kulevya. Tunajaribu kuangalia matatizo makubwa ya UKIMWI yanaanzia wapi, tumejaribu kuzunguka na kuongea na wadau mbalimbali wakatushauri na kutuambia na sisi wenyewe kwa kuona kwa macho matatizo ya UKIMWI yanaanzia kwenye ulevi. Kuna ulevi wa aina nyingi, kwanza mirungi, viroba, bangi, watakapokunywa na kuvuta wanajisahau wanaingia kwenye ngono zembe. Kwa hiyo, angalieni sana UKIMWI unaanzia wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali iweke utaratibu mzuri kutoa elimu ya UKIMWI kuanzia chekechea, shule za msingi, sekondari mpaka vyuo vikuu waelezwe UKIMWI unaanzia wapi na ni tatizo gani. Serikali ipange utaratibu wa kutoa elimu kwenye shule za msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali na hii bajeti ambayo imesomwa na Waziri Mkuu kuhusu shilingi milioni 50. Nategemea kwangu kupata shilingi bilioni 3.2, naamini kabisa ikitolewa elimu nzuri kwa hawa ambao wanalengwa, watanyanyua vipato vyao lakini kwanza wapewe elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri. Halmashauri yangu ina vipato vingi lakini vidogovidogo lakini mapato yale hayakusanywi. Kwa nini hayakusanywi? Wanatumia stakabadhi za kuandika kwa mkono. Naomba zile mashine zisambazwe katika Halmashauri zote…
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umemaliza, naomba ukae.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja asilimia mia moja kwa mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza kuunga mkono hoja hii.Wilaya ya Nyang’hwale haina Mahakama ya Wilaya na jengo la Mahakama, wananchi wanafuata huduma hiyo Geita umbali wa kilomita 180 kwenda na kurudi. Kwa hiyo,ni gharama kubwa hadi kesi kuisha na wengine kushindwa kumudu gharama za kwenda mara kwa mara Mahakamani hadi kufutwa kwa kesi na kukosa haki zao. Je,ni lini Serikali itaanzisha Mahakama ya Wilaya ya Nyang’hwale? Je,ni lini Serikali itaanzisha ujenzi wa jengo la Mahakama Wilaya ya Nyang’hwale?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza naanza kumshukuru mwenyenzi mungu ambaye amenijalia afya njema kwa siku ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kumwambia Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, kwamba sitaunga mkono hotuba hii mpaka hapa atakaponipa majibu yaliyo sahihi. Kwa nini nasema hivyo, leo mimi ni Mbunge katika Jimbo la Nyang‟hwale nina umri wa miaka sita katika nafasi hii ya Ubunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2010 Mheshimiwa Rais aliyepita wa Awamu ya Nne alikuja kuomba kura kwenye Jimbo hilo la Nyang‟hwale, akatuahidi kutujengea barabara kwa kiwango cha lami kutoka Kahama kupita Wilaya ya Msalala, Nyang‟olongo, Bukwimba, Nyang‟hwale, Busolwa, Busisi na Sengerema kwa Mheshimiwa Wiliam Ngeleja. Mwaka 2012 Mheshimiwa Rais alikuja kwa mara ya pili akiwa ameongozana na Waziri Mheshimiwa Jumanne Maghembe, Rais wa sasa, Mheshimiwa Majaliwa na Mheshimiwa Stephen Masele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuja akafanya mkutano wa hadhara pale, akatuahidi tena neno lile lile, kwamba nitawajengea barabara ya kiwango cha lami kutoka Kahama - Nyang‟hwale kuunganisha Sengerema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2015 mgombea Urais, Makamu wa Kwanza wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan naye alikuja akasema maneno yale yale. Tulimuomba na akasema barabara hii itajengwa kwa kiwngo cha lami. Mwaka 2015 Rais wa Awamu ya Tano Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli niliomba na kukumbusha na akasema mimi nilikuwa Waziri wa Ujenzi kipindi kile, sasa nikiwa Rais barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi waliamini na wakatoa kura nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais na mimi mwenyewe Mbunge. Leo nina sababu gani ya kuunga mkono hoja hii, viongozi wangu Wakuu wa Kitaifa wametoa ahadi na ahadi hii haimo ndani ya hiki kitabu, naunga mkono nini? Ninaomba Mheshimiwa Waziri, utakapokuja kuhitimisha hapo, bila kutoa majibu sahihi leo sikubali kuunga mkono na nitashika shilingi, itakuwa ni mara yangu ya kwanza leo. Huyo anayesema hawezi sijui yeye ndiye aliyenileta Bungeni? Mimi nasema sitounga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna lami ambayo tuliahidiwa, ujenzi wa barabara ya lami kutoka Geita kuja Nyang‟hwale yenye urefu wa kilometa 80, tangu mwaka 2013 tumeweza kujengewa kilometa sita. Kwenye kitabu hiki leo nimesoma nimepangiwa kilometa 2.78, kilometa 80 zitajengwa baada ya miaka mingapi? Nina haja gani ya kuunga mkono hoja hii? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ninaomba leo uniambie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niende kwenye upande wa mawasiliano. Jimbo langu lina Kata 15, lakini ni Kata sita tu ndizo zenye mawasiliano. Kata tisa ambazo ni Bukwimba, Kafita, Nyugwa, Kakola, Nyamtukuza, Nyabulanda, Shabaka, Nyijundu, Kaboha hazina mawasiliano ya simu. Lakini cha ajabu kwenye kitabu chenu hiki mmesema hivi; Busolwa kuna Mnara lakini haujawashwa, kuna kama Kata sita ziko hapa pembeni mmeonesha kwamba haujawashwa. Hebu niambiwe sababu gani kwa nini minara hiyo haijawashwa na iko tayari leo zaidi ya miaka miwili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wananchi wa Jimbo la Nyang‟hwale wanamsikiliza leo Mbunge wao, hawamuoni kwenye tv lakini wanamsikiliza kwenye redio kwamba leo Mbunge wetu…
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante, muda wako umekwisha ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, naanza kwa kuunga mkono hotuba ya Waziri. Pia naipongeza Serikali kwa mipango yake mizuri ya kusambaza umeme nchi nzima hata huko vijijini ili kuchochea maendeleo kwa wananchi na kuongeza pato la Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Nyang‟hware lina kata 15 na vijiji 62 hadi leo hii ni kata mbili zimefikiwa na umeme, nazo ni Kata ya Khalumwa na Nyang‟hware. Hata hivyo, Kata ya Khalumwa ndipo yalipo Makao Makuu, ni Kijiji kimoja tu ndiyo kina umeme. Pia Kata ya Nyang‟hware ni kijiji kimoja tu ndiyo umeme umefika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Busolwa tayari line imeshafika, lakini umeme haujawaka. Pia Kata ya Nyijunau nyaya za umeme zimepita juu kuelekea Kata ya Nyang‟hware ila Nyijundu haina umeme. Kata ambazo hazina kabisa umeme ni hizi: -
Kata ya Bukwimba na vijiji vyake; Kata ya Nundu na vijiji vyake; Kata ya Izunya na vijiji vyake; Kata ya Kafita na vijiji vyake; Kata ya Kakora na vijiji vyake; Kata ya Nyijundu na vijiji vyake; Kata ya Busolwa na vijiji vyake; Kata ya Kaboha na vijiji vyake; Kata ya Shabaka na vijiji vyake; Kata ya Mwingiro na vijiji vyake; Kata ya Nyaburanda na vijiji vyake; na Kata ya Nyamtukuza na vijiji vyake.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, tukiipitisha bajeti hii umeme upelekwe kwenye kata hizo, nitashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri sana. Katika hotuba nimeona kwa Wilaya ya Nyang’hwale tumejengewa nyumba za askari wetu kwa familia saba. Naomba kwenye bajeti hii tujengewe mahabusu kwani iliyopo imezidiwa, imekuwa ndogo sana sababu kuu ni kuwa na Makao Makuu ya wilaya.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa hotuba yao nzuri sana. Pia naipongeza Serikali kwa kutimiza baadhi ya ahadi zake, hasa kwenye miundombinu ya barabara. Kwa Wilaya ya Nyang’hwale kuna barabara mbili za TANROADs, moja inayotoka Wilaya ya Geita – Nyang’hwale na ya pili inayotoka Busisi – Sengerema – Nyang’hwale – Kahama hizi zina hali nzuri kwa sababu zina matengenezo ya kila mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukumbusha kwamba kuna ahadi ambazo ziliahidiwa katika Kampeni ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne mwaka 2010. Katika ahadi hizo ni pamoja na kuijenga barabara ya kutoka Kahama - Nyang’holongo – Bukwimba – Karumwa – Nyijundu
– Busolwa – Ngoma – Busisi Wilayani Sengerema; kwa kiwango cha Lami. Kifupi kutoka Kahama – Nyang’hwale – Sengerema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alipokuja kujinadi katika Jimbo la Nyang’hwale aliahidi pia kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; napenda kujua, je ni lini upembuzi yakinifu utaanza na kukamilika? Swali la pili; je ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza na kukamilika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia. Kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya njema na kuweza kusimama Bungeni hapa leo na kuweza kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri Ummy na Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa hotuba yao nzuri ambayo wameiwasilisha leo. Napenda pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kutupatia gari la wagonjwa katika Kituo chetu cha Afya Nyang’hwale. Mwaka 2017 tulipata gari moja na nashukuru mwaka huu tumepata gari lingine, hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Nyang’hwale kituo cha Afya na Hospitali ya Wilaya ya Nyang’hwale, ama Wilaya ya Nyang’hwale kwa ujumla tuna upungufu mwingi katika vituo vyetu vya afya na hospitali. Upungufu wenyewe ni kama ufuatao:-

Tuna upungufu wa dawa, Wauguzi, Madaktari na vifaa tiba. Vifaa tiba kama vile X-ray na Ultra Sound. Upungufu huu unasababisha wananchi wetu kupata usumbufu mkubwa kufuata huduma hizi Mkoani Geita. Kwa hiyo tunamwomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia upungufu huu ili kuwapunguzia adha wananchi wetu kufuata matibabu Mkoani Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bima ya afya. Watu wengi wamekuwa hawaoni faida ya bima ya afya sababu ni ipi. Sisi Wabunge tunajitahidi sana kuwahimiza wananchi wajiunge na bima ya afya, lakini wanashindwa kujiunga kwenye bima ya afya kwa sababu kwa wananchi ambao wameshajiunga na bima ya afya hawaoni faida yake. Vipi hawaoni faida yake? Ni kwamba wanapokwenda hospitali wanapata huduma, lakini huduma ya dawa wanakuwa hawaipati wanaambiwa waende wakanunue dawa hakuna dawa. Kwa hiyo hii inawafanya wananchi wakate tamaa kubwa ya kujiunga na huduma hii ya bima ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alifika katika jimbo letu na akaahidi Kituo cha Afya cha Kalumwa kiwe hospitali ya wilaya, lakini mpaka leo hii hatuoni mpango wowote wa Wizara kutupa hati ya kuipandisha hadhi kukipandisha hadhi kuwa Hospitali ya Wilaya ya Nyang’hwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa hospitali hii ipandishwe hadhi ili tuweze kupata dawa kulingana na wilaya; kwa sababu hospitali hiyo inahudumia vijiji zaidi ya 110, lakini pia wilaya za jirani zinakuja kupata huduma katika hospitali hiyo. Kwa hiyo kituo hicho kitakapopandishwa na kuwa hospitali ya wilaya naamini kabisa bajeti yake itakuwa ni kubwa na inaweza ikakidhi angalau kidogo kupunguza makali ya mahitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba wizara ijaribu kuangalia. Tuna wodi moja pale ambayo ilijengwa mwaka 1958. Wodi ile inalaza wagonjwa 10 tu na leo hii hospitali ile inapokea wagonjwa wengi sana. Kwa hiyo tunaomba sasa tuweze kujengewa wodi ambayo ni ya kisasa na inaweza kubeba wagonjwa walio wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Wizara kwa mikakati yake ya kupambana na ugonjwa wa saratani ya shingo ya uzazi. Ukweli ni kwamba naipongeza Serikali kwa kuanza kutoa chanjo kwa ajili ya kukinga tatizo hilo. Pia naomba sasa Wizara ishuke kule chini iende kutoa elimu ili kuondoa ile imani potofu waliyonayo wananchi wetu, kwamba tutakapochomwa sindano hiyo huwezi ukapata tena mimba, wengi wanaelewa hivyo, kwa hiyo naomba elimu hiyo iende ikatolewe kule chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Waswahili wanasema kinga ni bora kuliko kutibu. Kwa nini nasema hivyo; Wizara imeshagundua tatizo la chanzo cha ugonjwa wa saratani ya shingo ya uzazi. Jana nilisikia kwenye majibu ya Mheshimiwa Waziri hapa alisema kwamba chanzo chake ni kwamba inatokana na kuambukizwa na wanaume ambao hawajakata govi zao. Kwa hiyo naiomba sasa Wizara iende ikatoe elimu kwa walio na govi hizo ili waweze angalau zitolewe kuwakinga hawa. Kwa lugha nyingine wanaume ambao hawajafanyiwa tohara. Kwa hiyo naomba itolewe elimu kule ili kuweza kuwakinga hawa akinamama na maambukizi haya ambayo yanatoka kwa akinababa ambao hawajafanya tohara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naanza kumpongeza Waziri kwa hotuba yake nzuri ya matumaini makubwa kwa Watanzania. Pia naipongeza Wizara ya Afya kwa juhudi zake za kuhakikisha kuwa Watanzania wanakuwa na afya bora wakiwemo wananchi wa Nyang’hwale.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kama Mbunge kwa Wizara hii ni kuhakikisha pesa zinakwenda kwa wakati katika hospitali, vituo vya afya na zahanati zetu. Wizara imepanga kutoa chanjo kwa watoto wa kike ya saratani ya shingo ya kizazi. Kikubwa elimu itolewe huko vijijini ili wananchi waondokane na hofu ya chanjo hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu; Kituo cha Afya Kharumwa kina upungufu wa wataalam wa afya, vifaatiba, X-ray na kadhalika, pia dawa hazitoshi, wodi hazitoshi na zilizopo ni ndogo sana zina vitanda vinane kwa wanaume na wodi ya mama na mtoto ina vitanda 20 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Nyang’hwale vitambulisho vya wazee bado hawajapewa, kwa hiyo hawapati haki yao ya matibabu bure. Je, ni lini watapewa vitambulisho vyao?

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua kali zichukuliwe kwa watu wanaonajisi na kubaka watoto wadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kutoa gari la wagonjwa Kituo cha Afya Kharumwa. Wananchi wanawapongeza sana na wanaomba kwa Mungu muendelee na moyo huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri ni lini Kituo cha Afya Kharumwa kitapandishwa na kuwa Hospitali ya Wilaya? Hadi sasa inaitwa Hospitali ya Nyang’hwale lakini haijapata hati hadi leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja bajeti hii ya Wizara.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, naanza kwa kuipongeza hotuba ya Waziri wa Madini. Pia nwapongeza Waziri na Naibu wote wa Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa ushauri wangu kidogo kuhusiana na upotevu mkubwa wa mapato yatokanayo na madini ya dhahabu. Mfano, kuna wachimbaji wadogo Wilayani Nyang’hwale ambao wanachimba na kupata dhahabu bila ya kulipa mapato ya Serikali. Sababu kuu ni kutowapatia leseni ya uchimbaji au kutowatambua lakini yako maeneo mengi yanayochimbwa kama Kijiji cha Chibaranga, Ifugandi, Bululu, Isonda, Nundu, Nyamalapa, Iyenze, Ujulu, Isekelinyugwa, Nyijundu na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, kwa kuwa Wilaya ya Nyang’hwale haina maeneo yaliyopimwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Maeneo niliyoyataja yapimwe na kutolewa leseni ili Serikali iweze kukusanya mapato kirahisi pia kuwaepusha wachimbaji kusumbuliwa na kuhamahama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri sana ambayo imeonesha mafanikio mengi sana ambayo yamefanyika nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kutoa elimu bila malipo. Changamoto nyingi zimejitokeza kama upungufu wa vyumba vya madarasa, madawati, vyoo, nyumba za walimu, walimu na vitabu vya kujifunzia na kujifunza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kuboresha afya za Watanzania nchini. Upande wa afya Jimboni kwangu kuna baadhi ya changamoto kama vile upungufu wa wahudumu katika vituo vya afya na zahanati zetu. Pia katika vituo vyetu vya afya hatuna mashine hata moja ya picha ya X-ray na baadhi ya vifaa muhimu vya uchunguzi wa afya ya binadamu. Pia kuna upungufu mkubwa wa vitambulisho kwa wazee kwa ajili ya matibabu bure kwa wazee. Ni wazee 100 tu kati ya 6,000 ambao wana vitambulisho nchini, sasa hawa wazee 5,000 watapatiwa vitambulisho hivyo lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kuboresha baadhi ya kero kwa upande wa madini. Kwa upande wa Jimbo la Nyang’hwale bado kuna kero kubwa kwa wachimbaji wadogo kwa kutopimiwa maeneo yao na kupatiwa leseni za uchimbaji. Maeneo hayo ni Bululu, Ifugandi, Isonda, Isekeli, Lyulu, Nyamalapa, Kasubuya, Rubando, Iyenze, Shibaranga na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kupunguza kero ya maji vijijini na mijini. Kwa upande wa Jimbo langu la Nyang’hwale, kuna mradi mkubwa toka chanzo cha Ziwa Viktoria kutoka Nyamtukuza, Kakora, Kitongo, Ikangala, Kharumwa, Iyenze na Bukwimba. Mradi huu umeanza tangu 2014 hadi leo 2019 hata tone moja la maji halijatoka na kusuasua kwa wakandarasi wanadai Serikali haijawalipa fedha. Nataka kujua tatizo liko wapi, ni Serikali kutowapa malipo au wakandarasi ni matapeli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kuboresha miundombinu ya barabara kwa viwango vya lami na changarawe. Kwenye Jimbo la Nyang’hwale kuna ahadi za viongozi wa nchi, kuna Rais wa Awamu ya Nne kuhusu ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami toka Kahama - Nyang’holongo – Bukwimba – Kharumwa – Nyijundu – Busorwa – Busisi. Pia Rais wa Awamu ya Tano naye aliahidi, je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja hii.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja zilizoko mbele yetu. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi kwa kuipata nafasi hii, nafasi adhimu kabisa. Nianze kwanza kabisa kwa kumpongeza Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kukubali kukaa na wadau wa sekta ya madini, nami pia ni mdau, mchimbaji mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nijikite kwanza kwenye ushauri, kwa sababu dakika tano ni chache. Kwanza niipongeze Kamati kwa kazi nzuri ambayo wameifanya ya kuyapitia yote tuliyoyapendekeza kwenye kikao tarehe 22; kwa kweli kazi nzuri wameifanya, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, naomba Serikali iyafanyie kazi haraka yote ambayo yamependekezwa na Kamati ili kuepusha utoroshwaji wa dhahabu na madini mengine. Kwa mfano ucheleweshwaji wa utoaji wa leseni. Ucheleweshwaji wa utoaji wa leseni unachangia sana utoroshaji wa madini kwa sababu kuna watu wanaifanya kazi bila kuwa na leseni Serikali haiwatambui, wanatorosha madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali ifanye haraka sana kuwatambua hawa wachimbaji wadogo wadogo na kuwarasimisha, kuwapatia leseni ili iweze kuwatambua na kuweza kukusanya kodi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu mwingine ni kwamba NEMC, OSHA, ZIMAMOTO na Madini waweze kukaa pamoja ili kuweza kurahisisha taratibu zote za kuweza kutoa vibali. Leo vibali vimekuwa na matatizo, NEMC anakuja kivyake, OSHA anakuja kivyake, Madini anakuja kivyake; leseni zinachelewa kutoka na zikitoka pia ni kwa gharama kubwa. Naiomba Wizara ya Madini ilishughulikie hili ili waweze kuweka center moja ya kuweza kuyashughulikia haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu mwingine ni kwamba, kuna maeneo mbalimbali; kwa mfano Wilaya ya Nyangh’wale, kuna maeneo makubwa ambayo yanafanyiwa uchimbaji mdogo mdogo lakini wachimbaji hawajarasimishwa mpaka hivi sasa. Nina maeneo kama manane ambayo wachimbaji hawa wadogo wanachimba kiholela, wanaharibu mazingira na pia Serikali haipati mapato. Naiomba Wizara iyarasimishe maeneo hayo ili kuweza kuwapa wachimbaji wadogo wadogo na kuwapatia leseni na kuwatambua ili Serikali iweze kukusanya mapato. Leo hii dhahabu nyingi inatoroshwa kwa sababu udhibiti haupo, Serikali inapoteza mengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, jana alikuwa akijipambanua hapa Mheshimiwa Wizara wa Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kingwangalla, anasema anachangia asilimia 27 kwenye Pato ya Taifa, lakini dhahabu na madini mengine yakiwekewa utaratibu mzuri, naamini kabisa itakuwa ni sekta ya kwanza kuchangia mapato makubwa sana katika Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu mwingine ni kuhusu rasilimali watu pamoja na vitendea kazi; Wizara hii ya Madini iongezewe, Serikali itoe pesa kuongezea hii bajeti ili iweze kupata hawa watendaji pamoja na vitendea kazi vya kutosha kama vile magari ili kuweza kuzunguka maeneo mbalimbali. Kwa mfano, ukiangalia leo Geita ina gari mbili ambazo nazo hazifai, lakini pia ina wafanyakazi 20 tu, lakini Geita inaongoza kwa uchimbaji wa dhahabu. Je, wale watumishi 20 watawazungukia vipi wale wachimbaji wadogo na kuweza kukusanya maduhuli ya Serikali? Naiomba Wizara iongezewe pesa ili sasa waweze kuajiri watu wengi na pia kuweza kupata vitendea kazi kama vile gari na vifaa vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nitoe ushauri, kwamba Wizara itengewe pesa ili iweze kujenga maabara katika Mkoa wa Geita, kwa sababu Mkoa wa Geita ni kitovu cha dhahabu, ijengwe maabara kubwa na kuweka vifaa mbalimbali kwa ajili ya upimaji wa dhahabu na mambo mengine mbalimbali yanayohusiana na masuala ya dhahabu. Kwa hiyo naiomba Serikali itenge fedha ili kuweza kujenga maabara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na la mwisho niliomba nichangie muda mrefu, sasa dakika tano hazitoshi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Nishati
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, kwanza naunga mkono hoja hii iliyo mbele yetu. Nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri sana na kwa wanavyojitoa katika kuwatumikia Watanzania na kuhakikisha kuwa Watanzania wanapata umeme vijijini kwa maendeleo yao; lakini pia kwa kutekelea Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, mkandarasi wetu Wilaya ya Nyang’hwale kasi yake sio nzuri sana ya kusambaza umeme. Sababu anazozitoa anadai kwamba yeye amekwamishwa na upungufu wa nyaya.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri, ili kuhakikisha usambazaji huu wa umeme kwa Wilaya ya Nyang’hwale tutatulieni tatizo hilo la nyaya kwa wakandarasi wako. Ukizingatia tunaenda kwenye uchaguzi wa Serikali za Mtaa na Uchaguzi Mkuu 2020.

Mheshimiwa Spika, pale Makao Makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale, yaani Khalumwa tayari umeme upo ila baadhi ya maeneo mengi ya Mji wa Khalumwa hayana umeme na sababu kuu ni upungufu wa nguzo na nyaya. Mheshimiwa Waziri nakuomba sana tutatulie mapungufu hayo, wananchi wako tayari kufunga umeme.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza kabisa, niweze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kunipa afya njema na kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kuipongeza kwanza hotuba ya Waziri Mkuu, imesheheni mambo mazuri. Serikali yetu imefanya kazi vizuri, labda tu kabla sijaingia kwenye kuchangia, wachangiaji wawili waliotangulia, wamesema maneno mengi lakini hakuna hata neno moja la maana kwa sababu hotuba ya Waziri Mkuu imeonyesha mafanikio ya nchi hii. Cha ajabu wao kazi yao ni kuponda kila jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukawa una macho lakini huoni, unaweza ukawa una masikio lakini husikii. Cha ajabu ni kwamba hawa watani zetu wa jadi walisema mzigo mzito mpe Mnyamwezi na Mnyamwezi ameubeba mzigo huo na amefanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo ameifanya. Nadhani pia wanazidi kumkufuru Mungu kwa sababu hakuna mwanadamu aliyekamilika, lazima mwanadamu awe na upungufu. Kilichotakiwa ni kueleza mafanikio ya Serikali, lakini pia kuishauri maeneo ambayo yana upungufu kidogo. Kwa hiyo, ndugu zetu hao kazi yao ni kulalamika na wanasema 2020 tutakuwa na jeshi gani la kuweza kumudu uchaguzi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawahakikishieni kwamba uchaguzi wa 2020 asilimia kubwa ni CCM. Wananchi wanashuhudia Serikali ya CCM ni kazi ipi ambayo inafanywa nitazungumza kazi nzuri ambazo zimefanywa kwa kipindi cha miaka minne. Serikali ya Chama cha Mapinduzi imeweza kuanzisha elimu ya msingi bila malipo hadi sekondari. Hayo ni mafanikio mazuri na wananchi ni mashuhuda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna upungufu kidogo katika elimu ya bure. Tunaishauri Serikali ijaribu kuiangalia huo upungufu kwa sababu wimbi la wanafunzi kuandikishwa na kuingia mashuleni limekuwa kubwa. Pamekuwa na upungufu kidogo wa madarasa, madawati, Walimu na vyoo. Huu ndiyo ushauri tunatakiwa tuishauri Serikali ijaribu kuangalia na kuboresha maeneo kama hayo. Siyo kukaa mnalalamika kwamba Serikali haijafanya lolote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajaribu kuzungumzia kwenye upande wa afya. Serikali imeweza kupunguza gharama za wagonjwa kuwapeleka nje, imeweza kuboresha Hospitali zake za Rufaa, tumeweza kujenga shule, kujenga Hospitali nyingi za Wilaya na Vituo vya Afya. Leo hii tumeweza ku-save pesa nyingi za kuwapeleka wagonjwa wetu nje. Hiyo ni kazi ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tujaribu tu kuangalia upungufu kidogo uliopo. Mfano, katika Wilaya yangu ya Nyang’hwale, vifaa vipo lakini tumepungukiwa kama vile x-ray. Hatuna x-ray. Naiomba Serikali iweze basi kutuletea x-ray katika Kituo chetu cha Afya pale Kaluma. Huu ni upungufu lakini kazi kubwa imefanywa, dawa zipo za kutosha, majengo mazuri yapo na madaktari wapo pamoja na kwamba hawatoshelezi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijaribu kuzungumzia upande wa madini. Upande wa madini naipongeza Serikali imeweza kuweka utaratibu mzuri kuwasaidia wachimbaji kuondoa kero zao. Bado naiomba Serikali, kuna upotevu mkubwa sana ambao unapoteza mapato ya Serikali kwa kuchelewa kuwapa maeneo ya wachimbaji wetu kutoa leseni na kuweza kuwatambua. Kwa sababu wachimbaji walioko wengi sana katika Wilaya ya Nyang’hwale hawajarasimishwa na hawana leseni. Kwa hiyo, upotevu ni mkubwa na Serikali wala haiwatambui. Naiomba Serikali sasa iweze kuwatambua hao wachimbaji wadogo kwa kuwapatia leseni ili waweze kutambulika na waweze kuikusanyia Serikali mapato mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Nyang’wale, Serikali imefanya kazi nzuri sana, lakini kuna upungufu kidogo. Tuna mradi wetu mkubwa wa maji ambapo mradi ule umetengewa takribani shilingi bilioni 15.5, lakini mradi huo leo una zaidi ya miaka minne haujakamilika. Wakandarasi wako kazini wanailalamikia Serikali yao kwamba inawacheleweshea malipo. Nataka nijue, ni kweli Serikali inachelewesha malipo ama Makandarasi ni matapeli? Naomba nipate majibu wakati Waziri atakapokuja kufanya majumuisho hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mapambano dhidi ya Ukimwi, nilikuwa nataka nitoe ushauri. Serikali inatoa fedha nyingi sana kupambana na suala hili la Ukimwi. Suala hili tujaribu kuliangalia. Nataka nitoe ushauri, nitakuja kuchangia zaidi kule mbele. Kuna masuala ambayo yanasababisha kuongezeka. Pamoja na kwamba tunapambana, lakini bado kuna maeneo ambayo yanatakiwa yafanyiwe kazi. Mfano, kuna magulio maeneo mbalimbali hapa nchini. Magulio haya yanaanza saa 10.00 jioni na yanakwenda…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wetu ndiyo huo.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu kwanza naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kunipa afya njema. Lakini pia napenda nimpongeze Waziri pamoja na Naibu Waziri niwapongeze pia watendaji wote wa Wizara ya Maji. Pia nipende kuipongeza Serikali kwa kututengea pesa katika bajeti hii nimeona ukurasa 123 tumeweza kutengewa karibu 900,066,000.8. Lakini pia nipende kuishukuru Serikali kwa kuwalipa wakandarasi wetu zaidi ya bilioni 1.7 na sasa hivi tayari wapo kazini naishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizo cha ajabu ni kwamba Serikali ilitutengea mradi huu mkubwa wa kutoka Nyamtukuza kwenda Bukwimba mradi huu ulitengewa zaidi ya bilioni 15. Mpaka sasa hivi zimeshatoka takribani bilioni nane lakini cha ajabu kazi inavyoenda mpaka sasa hivi ninavyoongea hakuna hata tone moja ambalo linatoka la maji na mradi huu unagusa vijiji vinane, vijiji hivi ikiwa ni kutoka kule Nyamtukuza kwenye chanzo cha maji, panaitwa Nyamtukuza kupita Kakola, Kitongo, Ikangala, Kalumwa, Izunya, Kayenze na Bukwimba lakini mpaka leo hii hata tone moja la maji halijatoka,.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali pamoja na kutoa fedha zaidi ya bilioni nane ebu jaribuni kufuatilia mkaangalie huu mradi, huu mradi tangu mwaka 2010 naupigia kelele tangu 2010 mpaka leo hii mradi huu haujatoa hata maji kidogo. Bahati nzuri hata Mheshimiwa Mbalawa kipindi kile alikuwa Waziri wa Maji nimeenda naye mpaka kwenye chanzo cha maji. Waziri Mkuu amefika kule kwenye chanzo cha maji, eeh! Ndiyo kipindi kile alichokuwa waziri maji tumeshawahi kwenda naye, Mheshimiwa Eng. Kamwele tumekwenda naye mpaka kule na baadhi ya viongozi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha ajabu kuna mdudu gani ambaye anasababisha maji yasitoke nakuomba Mheshimiwa Waziri kwenye Bunge hili kabla ya kuhisha twende pamoja ukaone tatizo ni nini kwa sababu wananchi wa Nyangwale wanashida kubwa sana ya maji, mradi huu bilioni nane hata tone la maji halijatoa kwanini. Kwa hiyo, naungana kabisa na Wabunge wenzangu kwamba ufuatiliaji unakuwa ni mdogo, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba utakapokuja hapa uniambie ni lini mimi na wewe tuondoke twende tukaangalie huu mradi tatizo ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia niipongeze Serikali kwa mradi wa pamoja na Bulyang’ulu Acacia mradi huu ambao umegharimu takribani bilioni 13 naishukuru sana Serikali kwamba tayari imeshatenga fedha na wakandarasi wapo kazini mradi huu unatoka kwenye bomba kuu linalokwenda Kahama kwenda Irugi. Nimepata takribani vijiji saba ambavyo vitapitiwa na mradi huo kwa kweli naipongeza Serikali mradi huo utakapokamilika basi baadhi ya vijiji hivyo saba ambavyo nimevitaja vinaweza kupata maji, ambavyo ni vijiji vya Iyugwa, Tarumwa, Mwamakiriga, Izunya, Kavita pamoja na Lushimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumzia hili suala kwa uchungu sana ni kwanini kwa sababu kila ninaposimama miaka yote nazungumzia huu mradi wa Nyamtukuza, leo nazungumza taratibu sana mnielewe, sitaki kuzungumza kwa kasi na kwa haraka nizungumze taratibu mnisikilize vizuri, naomba Waziri twende pamoja tukaangalie mradi huu nini ambacho kinakwamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nimeona kwenye kitabu chako Serikali kwamba Serikali ya Oman na Serikali ya Tanzania wamekubaliana kuchimba visima mia moja, katika visima hivi ambavyo vitachimbwa kwenye shule za msingi na sekondari na Wilaya ya Nyang’hwale naomba basi niangaliwe angalau sekondari nne ambazo zinashida sana maji kama vile Nyang’hwale sekondari, Msalala Sekondari, Bukwimba Sekondari, Mwingiro Sekondari naomba angalau nipate visima vinne hivi ambavyo tunachangiwa na Serikali ya Oman. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna bwawa moja kubwa sana ambalo lipokule Kata ya Shabaka kijiji cha Nyamgongwa, bwawa lile lilikuwa kubwa sana na lilikuwa linanufaisha zaidi ya kata tano bwawa limeshaaribika takribani miaka thelathini na tano miundombinu yake imearibika lakini manufaa makubwa yalikuwa yanapatikana kwenye lile bwawa. Wananchi wengi walikuwa wakilima bustani walikuwa wakivua samaki, walikuwa wakilima kwa kumwagilia na manufaa mengine mbalimbali yalikuwa yanapatikana kwenye hilo bwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa ninaomba basi itengwe pesa kwa ajili ya kwenda kulitengenezea miundombinu bwawa lile liweze kuwasaidia wananchi, wananchi waweze kupata maji na kujipatia mapato, lakini pia mifugo kuweza kupata maji. Kwa hiyo, naomba katika bajeti hii angalau itengwe hiyo pesa kwa ajili ya hilo bwawa la Shabaka kijiji kimoja kinaitwa Nyamgongwa ambako amezaliwa ndugu yetu nimemsikia yuko hapa anaitwa Luhemeja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia baada ya kuyasema haya kuna kisima kirefu ambacho kimechimbwa katika Kata ya Nyangwale, Kijiji cha Nyang’hwale kisima kina miaka kumi na moja, miundombinu pale ilishakamilika Jengo lipo pump ipo, lakini cha ajabu maji mpaka sasa hivi hajaanza kusukumwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejaribu sana kufuatilia halmashauri wanasema wao hawana fedha kuna upungufu kidogo. Nilikuwa naiomba Serikali ikaiuangalie huo mradi ukamilishwe ili huo mradi uweze kusaidi kupunguza tatizo la maji katika Kata ya Nyang’hwale lakini pia vijiji vingine ambavyo vipo pale jirani kwa sababu ni kisima kirefu na kinamaji mengi sana. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri mchango wangu ni huo hauna maneno mengi kikubwa nakuomba tu ukautembelee mradi wangu wa Nyang’hwale ili uweze ku- pump hiyo hela na kuangalia tatizo nini ili sasa na mimi wananchi wangu waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu. Pia napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu Mawaziri na watendaji wote kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya katika Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo moja ambalo natakiwa nianze kulisema, leo ni mwaka wa nane niko Bungeni, kulikuwa na ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, aliahidi ujenzi wa barabara ya lami kutoka Kahama – Bukwimba – Nyijundu – Busisi Sengerema na Rais wa Awamu ya Tano naye pia ameahidi. Hata hivyo, cha ajabu kwenye kitabu hiki nimejaribua kuanzia ukurasa wa kwanza mpaka wa mwisho sijaona upembuzi yakinifu wa barabara hiyo. Kwa hiyo naomba nijue, ahadi za Marais hawa zimepuuzwa ama zitatekelezwa na kama zitatekelezwa ni lini? Kwa sababu barabara hii ina umuhimu sana, inaunganisha mikoa mitatu; inaunganisha Mikoa ya Shinyanga, Geita na Mwanza. Barabara hii ikifunguliwa uchumi wa Nyang’hwale utapanda. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri aingize angalau basi niweze kuona kwamba upembuzi yakinifu umeanza tuwe na matumaini, leo miaka nane nazungumzia barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, nimejaribu kuangalia kwenye kitabu chake, ameweza kunitengea karibu milioni 900 kwa ajili ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha changarawe kutoka Nyankumbu hadi Nyang’hwale, lakini kutoka Nyang’olongo mpaka Nyang’hwale. Barabara hii ina kiwango cha changarawe lakini imepangiwa kujengwa kwa kiwango cha lami kutoka Geita- Nyankumbu kuja Nyang’hwale. Cha ajabu, miaka nane imepita, lakini tumejengewa kilometa tano tu za lami na imesimama. Miaka miwili iliyopita hatukuweza kutengewa, je, 2019/2020 kwa nini tena haikutengewa ama imeondolewa kwenye utekelezaji? Naomba Mheshimiwa Waziri aiangalie barabara hiyo kwa sababu ilishaahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, kuna barabara ambayo ameiweka, barabara hii kwa kweli ikifunguliwa itakuwa imefungua maendeleo makubwa sana katika Wilaya ya Nyang’hwale. Ameweza kututengea pesa kufungua barabara ya wilaya kwa wilaya kutoka Mbogwe kuja Nyang’hwale; kutoka Bwelwa – Bukoli – Nyijundu mpaka Bumanda na Makao Makuu Kharumwa, Makao Makuu ya Nyang’hwale, barabara hiyo ikifunguka naamini mambo yatakuwa mazuri. Nimpongeze sana kwa hilo, naomba tu utekelezaji ufanyike kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Waziri anayehusika na masuala ya mawasiliano, kuna kata kama tano kwangu zina matatizo ya mawasiliano. Kata hizo zikiwa ni Shabaka, Nyamtukuza, Nundu, Nyabulanda na Nyugwa, mawasiliano sio mazuri, Mheshimiwa Waziri alitupa fomu tukajaza maeneo ambayo hayana mawasiliano mazuri, nami nilijaza ile fomu mwaka jana, lakini cha ajabu mpaka leo fomu hii haijafanyiwa kazi na wananchi wangu wanapata tatizo kubwa sana la mawasiliano. Namwomba Mheshimiwa Waziri atekeleze ahadi zake, aliahidi kwamba atashughulikia maeneo yote ambayo yana matatizo ya simu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kueleza hayo machache, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Kwanza kabisa kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nyang’wale, tunaungana na Wabunge pamoja na wananchi wote kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa tuzo ambayo ameipata na kuiletea heshima kubwa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli Mama anaupiga mwingi na anaupiga mwingi kweli kweli. Hapa sasa kwa lugha ya Kisukuma kama naruhusiwa kusema, wanasema “shirikalewa mnzengo hatina mangaka.” Maana yake ni kwamba, Askari wa Kijijini kwenu huwa hatishi, lakini Mama ametisha Kimataifa mpaka kupata tuzo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuendelee kumuunga mkono kwa mambo mengi aliyoyafanya kwenye miundombinu mbalimbali mfano ujenzi wa reli ya SGR, ujenzi wa bwawa la umeme, ujenzi wa madaraja, ujenzi wa miundombinu ya afya, ujenzi wa miundombinu ya kilimo na mambo mengine mengi. Mama ameupiga mwingi ndiyo maana amepata tuzo, nasi kama Watanzania tuendelee kumuunga mkono mama yetu kwa kazi nzuri anazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sina mengi yakusema, kwa niaba ya sauti ya wananchi wa Nyang’wale na Wabunge na Watanzania wote tuendelee kumuuga mkono Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, Katibu na Watendaji wote kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu nauelekeza upande wa wachimbaji wadogo hususan wa Wilaya ya Nyang’wale. Wachimbaji hawa mapato yanazidi kupotea, huwa nasema kila mara, lakini pia niipongeze Serikali ya Wilaya ya Geita ama Mkoa wa Geita kwa kuvuka malengo ya ukusanyaji asilimia 109. Hata hivyo asilimia hizo bado mimi nasema kuwa ni ndogo kwa sababu wachimbaji walio wengi mpaka sasahivi hawajatambuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, kuna wachimbaji katika maeneo ya Isekeli, Bululu, Ifugandi, Shibalanga, Rubando, Iyenze, Nyamalapa, Iyulu, Ibalangulu na Kasue. Maeneo yote yale, uchimbaji madogo mdogo unaendelea na ile dhahabu inapotea. Kwanini Serikali isichukue hatua ya haraka ya kwenda kuyapima yale maeneo ya kuwapa leseni wale wachimbaji wadogo ili tuweze kuwatambua na kuweza kupata yale mapato? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili ni kwamba kuna changamoto kwa wachimbaji wadogo wadogo wadogo na wadau wa madini katika Wilaya ya Nyang’wale kwa sababu tumeuwa hatuna Afisa Madini maeneo hayo na wachenjuaji wamekuwa wakipata gharama kubwa kwa kufuatilia vibali kutoka Wilayani Nyang’wale kwenda Geita. Kibali hicho unakifuata kwa gharama ya kilometa 180 kw akutumia trip mbili za gari. Trip ya kwanza ni kufuata kibali kwa ajili ya kuchukua carbon kuzipeleka Geita, na kibali cha pili ni kutoka pale Madini kwenda Ilusion, gharama zote hizo zinakuwa ni za mwenye carbon. Kwa hiyo ninakuomba Mheshimiwa Waziri, tufungulie ofisi ndogo ya Madini pale Nyang’wale tuweze kuepusha zile gharama kwa sababu gharama zinakuwa ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia bado tuna changamoto nyingine, tuna illusion zetu pale katika Wilaya ya Nyang’wale. Maafisa Madini wanakaa Mkoani Geita, ukitaka kuwafuata inabidi utumie gharama zako wewe mwenyewe kwenda kuwafuata. Hizo gharama tunaomba mtuepushie kwa kuwasogeza karibu hao Maafisa Madini pale Wilayani Nyang’wale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna urasimu mkubwa sana; Ofisi ya Madini Geita kuna urasimu. Unapofuatilia vibali ukifika pale unachukua zaidi ya masaa matatu kupewa kile kibali. Hicho kibali ni cha kwenda kuchukua carbon kutoka kwenye maeneo yako, kibali hicho ni cha kupeleka carbon pale madini. Lakini pia kibali kile cha kutoka madini kwenda illusion nacho unachukua zaidi ya masaa matatu kukipata kile kibali. Mimi nadhani utaratibu huu sio mzuri, jaribuni kuangalia utaratibu huo, haupendezi.

Mheshimiwa Spika, pia bado kuna urasimu mwingine. Unapomaliza kuchoma dhahabu yako pale kwenye illusion, TMA yuko pale, madini yuko pale na maafisa wengine wako pale wanakuandikia kibali hicho cha kubeba dhahabu yako kuipeleka kwenye soko; lakini bado utakapoibeba ile dhahabu ambayo labda umeipata gramu 100, utakapokwenda kwenye lile soko unakuta ofisi ya Tume ya Madini wanaipima tena ile dhahabu pale, ile dhahabu bahati mbaya ikitokea imepungua ilikuwa gramu 100 lakini wakaipima ikawa gramu 99 wanakusumbua kwamba gramu moja imekwenda wapi, ilhali kule kwenye illusion wamekuandikia gharama ya mrahaba na service levy iko kwenye karatasi. Kama imepungua si ni gharama yangu mimi acha ipotee hiyo? Lakini wana usumbufu na wanatisha watu, kwamba wameipeleka wapi.

Mheshimiwa Spika, suala hili sio zuri, urasimu huo sio mzuri. Dhahabu si cocaine, hii ni biashara. Jiulize huyu amepitaje hiyo dhahabu mpaka gramu 100 leo hii imepungua gramu moja, ni kipimo, vipimo vinatofautiana; lakini pamekuwa na usumbufu na vitisho. Kwa hiyo nakuambia Mheshimiwa Waziri, jaribu kuliangalia kwa Mkoa wa Geita, usumbufu huo upo. Kwa haya machache nakushukuru sana Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasiya kuweza kuchangia. (Makofi)
THE WRITTEN LAWS (MISCELLANEOUS AMENDMENTS) (NO. 4) ACT, 2021
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. Kwanza, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kuwa na afya njema na kuweza kusimama kwenye Bunge lako tukufu. Lakini pia, nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati Mheshimiwa Najma Giga pamoja na Katibu wake pamoja na Wajumbe wa Kamati kwa kazi nzuri ambayo tunaendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa AG pamoja na timu yake kwa ushauri mzuri na ushirikiano anaoutoa kwenye Kamati yetu ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kunipa katika Jimbo langu milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Kata ya Bukwimba kutokana na fedha ambazo zimekusanywa ndani ya miezi miwili kutokana na tozo la muamala. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. Pia, nampongeza kwa kusikiliza malalamiko ya Watanzania kuhusu tozo kubwa na kuweza kuipunguza kwa asilimia 30. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu ni mdogo sana. Kwa sababu umeshatupa maelekezo kwamba yale tuliyokubaliana na Serikali haina haja ya kuyarejerea. Lakini naomba tu uniruhusu kwenye upande wa posta nizungumze kidogo tu. Pamoja na kwamba tulikubaliana na Serikali…

SPIKA: Utakuwa unavunja maelekezo ya Spika. Kama wamekubali, kama kuna kipengele hawajakubali unaweza ukaendelea, lakini kama wamekubali haina sababu.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, walikubali. Lakini basi nitoe ushauri kwa AG kabla ya kuleta suala kwenye Kamati ya Katiba na Sheria akitaka kuleta jambo basi ni vyema waitwe wadau washauriane kwamba kuna suala hili ili liweze kuletwa ndani ya Kamati na kupunguza mlolongo wa maswali mengi kwenye Kamati.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Mambo yote yaliyozungumza ndani ya Katiba na Sheria tumeyapitisha, nimekubaliana na niipongeze Serikali, AG pamoja na Kamati yake kwamba tulikubaliana vizuri. Naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu hotuba mbili za Mheshimiwa Rais. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri za kuendelea kulitumikia Taifa letu, lakini pia mipango yake mizuri ambayo wananchi ilikuwa ni tarajio lao.

Mheshimiwa Spika, hotuba hizi mbili zimeligusa Taifa, lakini limegusa jimbo langu katika kila nyanja. Mheshimiwa Rais alizungumzia uboreshaji upande wa sekta ya elimu. Kwa kweli elimu inaendelea kuboreshwa na kuendelea kupunguzwa changamoto ambazo ziko katika maeneo mbalimbali kwenye shule zetu ikiwa ni pamoja na kuwaondosha watoto wetu kukalia matofali pamoja na mawe. Ametoa agizo Mheshimiwa Waziri Mkuu na tunaendelea kutekeleza kuhusu masuala ya wanafunzi wetu kukamilisha madawati pamoja na madarasa.

Mheshimiwa Spika, lakini bado kuna changamoto mbalimbali ambazo zinakabili sekta hiyo hususan upande wa Nyang’hwale Waziri wa Elimu alichukue hili kwamba tuna upungufu mkubwa wa walimu hasa wa sayansi. Pia bado tuna upungufu mkubwa wa nyumba za walimu pamoja na vitendea kazi. Mheshimiwa Rais alizungumzia suala la kupunguza kero ya akinamama kufuata maji mbali, kupunguza kero hiyo vijijini pamoja na mjini. Nashukuru kwamba sekta ya maji imepiga hatua kubwa ikiwemo Jimbo la Nyang’hwale, tuna mradi mkubwa ambao tulitengewa fedha zaidi ya bilioni 15.

Mheshimiwa Spika, mradi huu Waziri wa Maji atakuwa yupo, ajue kabisa kwamba mradi huu unakwenda kwa kusuasua, umechukua muda mrefu na tarajio kubwa la wananchi wa Nyang’hwale kupate maji kutoka Ziwa Victoria ni kiu chao kikubwa sana. Leo tumekuwa tukiahidiwa kwamba mradi huu utakamilika ndani ya miezi mitatu, ndani ya miezi miwili, lakini mradi huu haufikii mwisho. Wananchi wetu wanaenda wanapoteza imani kubwa na Wizara hii Maji kwa sababu ahadi hiyo inakuwa haikamiliki.

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu wamezungumzia mtoto huyu TARURA, TARURA fedha zake inabidi ziongezwe tumekuwa na changamoto kubwa sana ya barabara kwenye halmashauri zetu, lakini TARURA amekuwa hawezi kukidhi kurekebisha barabara hizo kutokana na uchache wa fedha. Kwa hiyo, naungana na wenzangu kwamba hoja hii ya kumwongezea mtoto huyu wa TANROADS, TARURA aweze kupata fedha kuweza kukidhi shida mbalimbali zilizoko kwenye maeneo hususani kwenye halmashauri zetu ikiwemo Nyang’hwale; barabara nyingi zimeharibika TARURA hawezi kutokana na kiwango kidogo cha fedha ambacho anapewa.

Mheshimiwa Spika, hotuba hizi zimegusa maeneo mbalimbali imegusa upande wa umeme, kuboresha umeme kuongeza uzalishaji wa umeme ili sasa tuweze kuwa na viwanda na umeme wa uhakika. Nampongeza sana Waziri wa Nishati, juhudi kubwa zinafanywa huko vijijini lakini bado kuna changamaoto. Nitazungumzia upande wa Jimbo langu, ni vijiji 62 lakini mpaka sasa hivi vijiji ambavyo vimeshawashwa havijazidi hata nusu. Yeye amesema hapa nilivyomsikia kwamba bado miezi michache vijiji vyote vya Tanzania vitakuwa vimekamilishwa umeme, sasa sijui na Nyang’hwale vitakuwa vimekamilika? Kwa hiyo, changamoto ya umeme Jimboni kwangu bado ni kubwa kuna maeneo mbalimbali nguzo zimesimikwa na mashimo yamechimbwa lakini waya ndiyo tatizo kubwa. Mkandarasi wetu kila unapoongea naye anasema tatizo kubwa ni la nyaya. Kwa hiyo, namwomba Waziri wa Nishati awasiliane na huyo mkandarasi aelewe tatizo ni nini. Si changamoto tu ya umeme kwa wilaya ya Nyang’hwale, ni maeneo mengi kwa hiyo, Waziri wa Nishati ajaribu sana kuangalia wakandarasi wake ili waweze kwenda na wakati.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana kwa kipindi cha miaka mitano ikiwemo kuimarisha usafiri wa anga, leo Tanzania tunajivunia usafiri wa anga, tuna ndege zetu ambazo zimeshakuja na zingine zinakuja na kwa kweli zimeleta faida kubwa, zimeleta sifa kubwa kwa nchi yetu, lakini pia Rais wetu kafanya kazi kubwa maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, muda wa hutoshi nataka nizungumzie suala la upande wa kilimo; wakulima wetu wamekuwa na changamoto nyingi ikiwemo pembejeo ambazo zinakuja mbovu, hazifai lakini changamoto nyingine kubwa ni soko la uhakika. Waziri wa Kilimo yupo, wananchi wetu mazao yao sasa hivi yapo hayana thamani, tunamwomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, ajaribu kuliangalia sana suala hili la kuzuia upelekaji wa vyakula nje, wananchi wetu leo hii wanahangaika kupata fedha kwa sababu ya zuio hilo la kuzuia kupeleka chakula nje.

Mheshimiwa Spika, najaribu kuangalia leo hii jimboni kwangu debe la mahindi mpaka sasa hivi linauzwa shilingi 7,000, mkulima huyu atatoka vipi hapo alipo debe la mahindi shilingi 7,000 lakini kama kungekuwa soko la nje naamini kabisa asingeweza kuuza debe la mahindi shilingi 7,000. Kwa hiyo, Waziri wa Kilimo ajaribu kuliangalia hilo zuio, sawa lina wakati wake hilo zuio, kama hali ya hewa ya chakula si nzuri, waweke hilo zuio, lakini kwa sasa hivi hali ya hewa ni nzuri na wakulima wetu wanapata vyakula kwa wingi ili waweze kutoka hapo, basi tunaomba soko hilo liweze kufunguliwa kuweza kupeleka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusu Mheshimiwa Rais alivyokaa na wachimbaji wa madini mbalimbali, kwa kweli hamasa imekuwa ni kubwa na pato la nchi limeongezeka, lakini bado kuna changamoto ziko kwa wachimbaji wetu wadogo wadogo. Nitazungumzia wachimbaji wadogo wadogo walioko Wilaya ya Nyang’hwale, wana maeneo ambao wameyavumbua lakini inakuwa ni tatizo kubwa la kuweza kuwapatia leseni. Kuna maombi mbalimbali ambayo yameombwa kwa wachimbaji wetu wadogo ili waweze kupatiwa maeneo ya uchimbaji lakini leseni zenyewe kutoka inakuwa ni changamoto.

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Madini kwa sababu yupo hapa namwomba sasa, wachimbaji wadogo wa Wilaya ya Nyang’hwale wamekuwa na changamoto ya kupata huduma za Ofisi ya Madini kwa sababu Ofisi ya Madini inakuwa iko mbali, zaidi ya kilomita 90. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Madini aweze kuangalia namna gani ya kufungua Ofisi ya Madini pale Makao Mkuu ya Wilaya ya Nyang’hwale Kharumwa ili hawa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini waweze kupata huduma hiyo karibu hapo na kuweza kusababisha kuzuia mianya saa nyingine ya kuweza kutorosha madini haya. Mtu anapotoka eneo moja kwenda eneo lingine inawezekana kuna jambo liko pale katikati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Madini naomba ulichukuwe hili ili uweze kuwasaidia wachimbaji wa Nyangh’wale kwa kuwasogezea huduma. Nimeshalizungumza sana suala hilo.

Mheshimiwa Spika, bila kukuficha Mheshimiwa Waziri wa Madini, Nyangwale wamemuunga mkono sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, sasa hivi utoroshaji wa madini asilimia 98 nakuhakikishia haupo tena. Kwa hiyo, nakuomba Mheshimiwa Waziri wa Madini hakikisha basi unaifungua hiyo ofisi ili kuweza kukamilisha zile asilimia 2 za wasiwasi unaweza kutorosha madini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya ardhi, Mheshimiwa Waziri wa ardhi yupo, wananchi wangu hususani wa Wilaya ya Nyang’wale wamekuwa wakienda kuomba kupimiwa ardhi zao pamekuwa na usumbufu mkubwa, njoo kesho, njoo kesho kutwa. Waziri wa Ardhi ajaribu kuwasiliana na Maafisa Ardhi wa Wilaya ya Nyang’wale ajue kwa nini wamekuwa wakiwasumbua wananchi kuhusu suala la kupima ardhi zao.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja iliyoko mbele yetu ya hotuba ya Mheshimiwa Rais, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mpango uliopo mbele yetu. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa nikiwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wenyewe kwa sababu ni dakika tano, nijikite sana kwenye ushauri na napenda Waziri wa Fedha ajaribu sana kusikiliza ushauri wangu. Mheshimiwa Rais alituita pale Ikulu sisi kama wafanyabiashara na wadau mbalimbali kutaka kujua changamoto tulizonazo kwenye upande wa biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulimwelezea changamoto zetu ikiwemo tatizo kubwa lililoko bandarini kuhusu TRA. TRA kule bandarini wana usiri mkubwa. Usiri huu unasababisha watu kukwepa kulipa kodi na tozo mbalimbali, lakini pia unasababisha kupoteza mapato makubwa ya Serikali. Mfano, leo hii utakwenda China ama mtakwenda China watu watatu ama wanne mnaofanya biashara ya aina moja, mnakwenda kununua mabegi kila mmoja container moja, lakini mnapofika bandarini kila mmoja analipa kodi tofauti na mwenzake, hii ni kwa nini? Wajaribu kuangalia usiri uliopo bandarini, kuna usiri mkubwa sana. Kama alivyosema yule mchangiaji mwingine, leo hii Mtanzania anaona bora kufuata mzigo Uganda na kuuleta Tanzania kuliko kufuata mzingo Dubai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Uganda mzigo unakuwa na bei ya chini kuliko Tanzania, wakati tumetumia bandari yetu, barabara yetu kusafirisha mzigo kwenda Uganda. Inakuwa hivyo kwa sababu hapa kuna utitiri wa mambo mengi, TRA wajaribu kuangalia tatizo hili lililoko bandarini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine nitautoa kwa pale bandarini. Leo hii unaingia dukani ama madukani, unaingia duka moja unakwenda duka linguine, unaingia kwenye duka hili mtu anakupa bei anakwambia hii ni ya risiti ya VAT; bei hii haina risiti haya yametokana na nini? Mwanzo wa kule bandarini. Biashara nyingi leo zimekufa kwa sababu kuna double standard ya kulipa kodi, nina Ushahidi, nimeingia duka moja nikaenda nikanunua mzigo wenye thamani ya milioni 35, nikapewa risiti ya milioni 1,500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikamwambia yule mama wewe hujipendi nipe risiti iliyo kamili, sheria gani inakulinda wewe ya kutoa risiti nusu, lakini cha ajabu ni kwamba mpaka leo hii mchezo huo upo na TRA walitangaza kwamba anayenunua ahakikishe anapewa risiti na anaomba risiti, cha ajabu leo hii mtindo huu wa kununua na kuuza hakuna anayetoa risiti. Fedha nyingi za mapato ya Serikali yanapotea, lakini cha ajabu, sheria hii hatujawahi kuipitisha Bungeni ya kwamba mtu akikamatwa hajatoa risiti ama amekamatwa amenunua na hakuomba risiti atatozwa faini ya kuanzia 30,000 mpaka 1,500,000, mambo haya yamepitishwa lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha ajabu leo hii kuna hawa Machinga (wafanyabiashara wadogo wadogo) wanauza bidhaa zenye thamani kubwa na hawatowi risiti, TRA hawaoni kama wanapoteza mapato? Nina ushahidi nimenunua brenda ya juisi ya shilingi 120,000 kwa mfanyabiashara huyu anayeitwa Machinga hajatoa risiti, lakini leo hii ukiingia supermarket hata ukinunua pipi unapewa risiti, wajaribu kuangalia sana TRA kuna maeneo wanapoteza mapato. Ushauri wangu wahakikishe wafanyabiashara kuanzia hao wadogo, wa kati na wakubwa waunganishwe kwenye mfumo wa ulipaji kodi EFD yaani wahakikishe kila mmoja anagawiwa hiyo mashine hata bure ili aweze kutoa risiti, tuna mapato mengi ambayo tunapoteza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikia Mheshimiwa Waziri anasema tumevuka malengo, sasa hivi tunakusanya trilioni mbili kwa mwezi. Kwa uzoefu nilionao kuna trilioni zaidi ya tano ziko kule nje, zinapotea hivi hivi. Namwomba Mheshimiwa Rais kama itampendeza, sisi wafanyabiasha ambao tunaitwa wa darasa la saba elimu, yetu ya msingi tumo wengi humu ndani, tunamiliki uchumi wetu, kama itampendeza achague angalau hata watu wawili hao wenye elimu ya darasa la saba wakawe Manaibu Waziri, upande wa Wizara ya Fedha ama Viwanda tuweze kuwashauri vizuri, haya tunayoyazungumza, kwa sababu tuko ndani ya field tunayaelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Musukuma alitoa ushauri na namuunga mkono kwamba TRA watengeneze vijarida ama vitabu vya kuonyesha uhalisi na uhalali wa kulipa kodi. Waende wakajifunze Uganda, kwa nini ukienda Uganda unataka kufuata gari, unataka kufuata TV unaambiwa na Mamlaka ya Mapato yao, ukileta TV yako utalipa bei hii. Mtu anakwenda kununua bidhaa yake kule nje anajua nikifika hapa nitalipa kiasi fulani lakini kwa TRA ya Tanzania kuna usiri mkubwa. Nasema TRA kuna usiri mkubwa lakini ni wachache siyo wote, nawapongeza wanafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba watangulize uzalendo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja, lakini na sisi wa darasa la saba muwe mnasikiliza michango yetu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kusimama hapa leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuunga mkono hoja iliyopo mbele yetu ambayo ni hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwa kweli imesheheni na imegusa maeneo yote, hususan kwenye maendeleo ya nchi yetu. Vile vile niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kipindi chake cha miaka mitano kuweza kutuingizia fedha nyingi za maendeleo katika Wilaya ya Nyang’wale zaidi ya shilingi bilioni 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuendelea kutekeleza yale yote ambayo yaliyoanzishwa na Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, tunamuunga mkono kwa nguvu zote Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, tuko naye bega kwa bega na ninawaomba Watanzania waungane na wananchi wa Nyangh’wale kuwalaani wale ambao wanayaponda na kuyapuuza mazuri yalioanzishwa na Hayati Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia maeneo machache sana. Namwomba Waziri wa Fedha na Waziri wa Viwanda mnisikilize vizuri. Kuna changamoto nyingi kwenye upande wa kodi na huwa nalizungumza kila mara, lakini hamlichukuli maanani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha anisikilize vizuri. Nimeshauri mara nyingi sana tupanue wigo wa kukusanya kodi. Kuna maeneo mengi sana tunapoteza kodi na mnasema wale ni wafanyabiashara wadogo lakini wanapoteza mapato ya Serikali. Mfano, ukienda Chako ni Chako pale, ukiangalia yule mtu anauza kuku zaidi ya 300 kwa siku moja, lakini mtu huyo hatoi risiti. Hilo ni eneo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, nilishasema kwamba TRA na wafanyabiashara kuna usiri mkubwa. Kwa nini nasema hivyo? Leo hii wafanyabishara wenye maduka, ushahidi ninao, nimeamua kujilipua Mheshimiwa Waziri wa Fedha, naomba unilinde; baadhi ya maduka, katika maduka 10, matatu tu ndiyo yanayotoa risiti. Maduka saba hayatoi risiti na ushahidi ninao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimekwenda kwenye duka fulani Dar es Salaam muda wa saa saba mchana, nikanunua bidhaa zaidi ya shilingi 200,000/=, wamenifungia mzigo. Wakati nataka kuondoka nikawaambia nipeni risiti, wanadai kwamba hapa tangu asubuhi anayetoa risiti hayupo. Mauzo kiasi gani Serikali imepoteza fedha pale? Naomba lifanyieni kazi. Kama utataka ushahidi zaidi, niko tayari kuvaa kofia na kanzu iliyoisha, niende na kuonesha maeneo ambapo upotevu wa fedha za Serikali upo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa ushauri kwa upande huo.Hakikisha kwamba unawasajili wafanyabiashara wa kati ama wafanyabiashara wadogo, wagawie zile mashine ya EFD ili waweze kutoa risiti. Nakuomba Mheshimiwa Waziri achukue ushauri mwingine, punguzeni VAT kutoka kwenye asilimia 18 na iende mpaka 13 ili watu waweze kulipa VAT. Huo ni ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme jambo lingine. Walipa kodi wa nchi hii juzi nilisikia ni takribani milioni 3.9, lakini kuna walipa kodi zaidi ya milioni 3.9 ambao hamjawasajili na wapo, fanyeni utafiti wa kina. Hizi fedha mnazosema mnakusanya shilingi trilioni mbili kwa mwezi ni kidogo sana. Mimi ni mfanyabiashara, ni mchimbaji, ninaelewa. Tuliweza kulisaidia Taifa kwenye upande wa madini, tulitoa ushauri na leo hii Waziri wa Madini yuko pale, anazungumza kwa kutamba, yuko vizuri, Wizara yake inakusanya pesa vizuri. Nakuomba Mheshimiwa tuiteni wafanyabiashara tuweze kusema yaliyoko kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania hao wafanyabiashara hawana nia ya kukwepa kodi ila kuna matatizo upande wa TRA. Tunaomba mtuite tuje tutoe ushauri. Pia hatuwezi kusema yote hapa; siwezi kumwaga mchele kwenye ndege wengi, kwa sababu kuna mapapa wapo ambao wanapoteza mapato makubwa ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa TBS. Leo hii ukienda Dubai ukaleta mzigo unaozidi dola 5,000, TBS watakupiga faini ya asilimia 15, lakini kuna watu wale mapapa wanaingiza makontena na hawatozwi hiyo TBS. Leo hii mnaenda kuwakamua hao watu wadogo, watu wachache lakini kuna mapapa wapo. Mheshimiwa nitafute kwa wakati wako na unilinde nitakupa siri za wafanyabiashara ambao wanapoteza mapato ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia mada iliyopo mbele yetu. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia afya njema kufikia jioni hii ya leo. Lakini pia nianze kumpongeza Waziri wa Madini Mheshimiwa Doto Biteko pamoja na Katibu wake Prof. Shukrani Manya na watendaji wote wa wizara. Lakini pia naipongeza hotuba na naiunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kuipongeza wizara kwa hotuba yake nzuri kwa kuelezea wingi wa leseni ambazo zimeshatolewa kwa wachimbaji wadogo nchini; ikiwemo wachimbaji wadogo wa Jimbo langu la Nyang’hwale. Kwa kweli leseni zimeshatoka PML zaidi ya PML 50 kwa hiyo, wachimbaji wadogo wa Nyang’hwale wanaipongeza sana wizara, Waziri pamoja na Naibu Waziri. Lakini pia ukweli usiopingika, madini yanaliingizia Taifa fedha nyingi, lakini pia tukumbuke madini kote yanakochimbwa kuna athari kubwa ya kimazingira. Nitatoa mfano kwenye jimbo langu la Nyang’hwale kulikuwa na msitu unaitwa Iyenze, kwasababu msitu ule umezungukwa na wachimbaji msitu huo miti yote imekwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaangalia namna gani tunavuna sasa hivi, lakini kizazi kijacho fedha hii ambayo tunaipata sasa hivi itarudi tena kwenda kuandaa mazingira. Nilikuwa nataka nitoe ushauri kwamba wizara iweke mpango mzuri wa kuweza kuwakopesha wachimbaji wetu wadogo ili waweze kupata zana za kisasa. Miti ile imekwisha kwenye ile misitu kwa ajili wanaitwa matimba; uchimbaji wowote wa dhahabu unahitaji matimba ni zile ngazi za kuingilia shimoni. Ukiangalia ule msitu wa Iyenze umekwisha na kuna msitu ambao ukitoka Geita unakwenda Katoro na wenyewe unakwenda kuisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ushauri wangu naomba sana wizara ijaribu kuangalia namna gani ya kuwasaidia wachimbaji hao wadogo waweze kupata zana hizi za matimba ama zana nyingine za uchimbaji ili kupunguza uhalibifu wa mazingira. Lakini ushauri wangu mwingine ni kwamba Wizara ya Madini ishirikiane na Serikali za Vijiji. Nimezungumzia uharibifu wa mazingira leo unakuta maeneo ya wachimbaji ama kwenye vijiji ambako kuna wachimbaji unakuta kila mchimbaji anatengeneza kitu kinaitwa mwalo Kijiji kizima unakuta kuna miyalo miyalo, na ile miyalo inatumika Zebaki ambayo ni sumu, sumu hiyo itakuja kuleta madhara makubwa kwenye kizazi kijacho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaiomba Serikali, naiomba sana wizara ishirikiane na Serikali za Vijiji kuangalia angalau maeneo maalum watakayofanyia hizo kazi zao hao wachimbaji kama ni kuharibika eneo liharibike eneo fulani tu. Sio sasa hivi kila mchimbaji, ukikuta kijiji kina wachimba 200 kila mmoja unamkuta ana mwalo kwake anatumia sumu hii ni hatari sana kwa maisha ya wachimbaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa waziri nimekupongeza sana, ni mmoja wao wa uanzilishaji wa masoko ya dhahabu. Kama unakumbuka kulikuwa na Kamati ya Naibu Waziri Stanslaus Nyongo mimi nikiwa makamu, tulianzisha na leo kila anayesimama anasema wilayani kwangu kuna duka la dhahabu. Ninakupongeza tulianza vizuri na tunaenda vizuri, tuendelee vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya Mheshimiwa, naunga mkono hoja. Ahsante kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia. Kwanza, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha mimi pamoja na sisi sote humu ndani kuwa na afya njema. Pia, nimpongeze Waziri na Naibu Waziri pamoja na Watendaji wa Wizara kwa hotuba yao nzuri sana.

Pia, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutoa elimu bure kwa wanafunzi wa shule za msingi pamoja na sekondari kwa nchi nzima, ikiwemo Wilaya ya Nyang’hwale ambayo imeweza kupokea fedha hizo zaidi ya bilioni tatu. Naipongeza sana Serikali. Pia, kuna changamoto mbalimbali nyingi, lakini nitazungumza chache.

SPIKA: Mheshimiwa Amar.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, naam.

SPIKA: Wenyewe wanaiita Elimu Bila Malipo kama sikosei, lakini siyo Elimu Bure. Watanisahihisha baadaye. Wanasema kuna tofauti kati ya vitu hivyo viwili.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nirekebishe kauli, Elimu Bila Malipo.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali imeweza kutuletea fedha zaidi ya shilingi bilioni tatu kwa ajili ya Elimu Bila Malipo upande wa shule za msingi pamoja na sekondari. Kuna changamoto nyingi kwenye upande wa elimu lakini nitazungumza chache, hususan kwenye upande wa Wilaya yetu ya Nyang’hwale.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa kwamba upungufu wa vyumba vya madarasa kwa nchi nzima upo, lakini nitazungumzia kwa upande wa Wilaya yetu ya Nyang’hwale. Tuna upungufu sana katika shule za msingi, mahitaji ya madarasa ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunahitaji madarasa 1,138, lakini yaliyopo ni 616, upungufu ni madarasa 522. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri hili alichukue, lakini nitakuwa na ushauri huko mbele. Pia, tuna upungufu wa madarasa kwenye shule zetu za sekondari zaidi ya vyumba 30, lakini pia tuna upungufu wa Walimu. Upande wa shule za msingi tuna upungufu wa Walimu 342 na upande wa sekondari tuna upungufu wa Walimu 180.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa ushauri kwa Mheshimiwa Waziri kwamba tumekuwa tukiandaa vijana wetu na wanapomaliza masomo ama kutokuendelea na masomo wanarudi mtaani. Mfano, vijana wetu wanaoshindwa kuendelea na elimu ya juu, wanarudi mitaani wanakuwa hawana kazi. Naomba kushauri kwamba Wilaya ya Nyanghwale tuweke utaratibu mzuri hapo mwakani Wizara iingize ndani ya bajeti iweze kutujengea Chuo cha Ufundi Stadi ili wale wanafunzi wanaoshindwa kuendelea na elimu ya juu, basi waweze kujifunza ufundi ili waweze kujiajiri wenyewe.

Mheshimiwa Spika, nataka nifikishe pia kilio cha Walimu wetu wastaafu. Kuna Walimu wastaafu wapatao 20, leo wana zaidi ya miaka sita wanadai mafao yao na wameshakuja hapa Dodoma nimewapeleka kwenye ofisi husika zaidi ya mara nne, wamehakikiwa.

SPIKA: Mheshimiwa rudia hiyo point yako, Waziri wa Nchi alikuwa hakusikilizi.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, kuna Walimu wastaafu zaidi ya 20, wakidai mafao yao zaidi ya miaka sita. Wamekuja hapa Dodoma nimewafikisha sehemu husika zaidi ya mara tatu, wanaambiwa tumeshahakiki subirini malipo yenu. Mpaka leo hii wamenipigia simu wanasema Mheshimiwa hatujalipwa mafao yetu na wengine ni wagonjwa, hali zao si nzuri. Naomba nilifikishe hilo kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, mwisho, naomba kutoa ushauri kama walivyoshauri wenzangu kuhusu wanafunzi wetu wanaotoka majumbani saa 12, wanarudi jioni wakiwa hawajanywa chai, hawajala chakula, naomba uwekwe utaratibu ulio mzuri ili wanafunzi wetu waweze kupata chakula. Kipindi cha nyuma kulikuwa na utaratibu huo wa kutoa chakula kwenye shule zetu, lakini pakawa na upotevu wa chakula ambacho kilikuwa kikilimwa na wale wanafunzi. Tujaribu kuweka utaratibu mzuri, Bodi ya Shule iwashirikishe wazazi pindi watakapokuwa wanalima wanafunzi chakula chao, wazazi na wenyewe washughulike kuhakikisha kile chakula kinatumia ipasavyo; ili wale wanafunzi wapate chakula. Nitatoa mfano, kuna vijana wa sekondari wanatoka eneo moja kwenda eneo lingine maili saba kwenda kusoma kuanzia saa 12 mpaka jioni, wanarudi wakiwa hawajala chakula. Nadhani hawatakuwa na mafanikio mazuri kuhusu elimu yao, ndio maana tunatengeneza vijana wengi ambao wanashindwa kuendelea na masomo yao.

Mheshimiwa Spika, sina mambo mengi ni hayo tu machache ya ushauri, lakini naomba suala la Walimu wangu wastaafu lichukuliwe kwa umakini, walipwe haraka fedha zao kwa sababu leo ni miaka sita wanafuatilia mafao yao.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Lakini kwanza naanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema pamoja na Wabunge wote pamoja na watumishi waliopo kwenye jengo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Waziri wa Wizara hii ya Maji, Mheshimiwa Jumaa Aweso, pamoja na Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Engineer Maryprisca Mahundi pamoja na Katibu wa Wizara, Engineer Sanga, na watendaji wengine wote. Kwa kweli wanafanya kazi vizuri, ninawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi hizi nizipeleke kwa Mheshimiwa Waziri, aliwahi kufanya ziara kwenye jimbo langu akiwa Naibu Waziri na ziara ile imezaa matunda na huu mradi ambao ulikuwa umekwama takribani miaka mitano unakwenda kukamilika; hongera sana Mheshimiwa Waziri. Kwa nini nampongeza; alivyokuja kule aliwatia pingu wale wakandarasi na kasi ikaongezeka; hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Naibu Waziri amefanya ziara hivi karibuni na kuona mradi wetu ulipofikia na akatia hamasa, na kuna fedha ilikuwa imepungua kidogo ameahidi kuipeleka ndani ya mwezi huu. Na Inshallah kufikia mwezi ujao mradi huu unakwenda kukamilika katika vijiji 12; hongera sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichangie machache sana. Mradi huu unakwenda kukamilika lakini wananchi walio wengi wa Jimbo la Nyang’hwale ambako umepita huu mradi wanahitaji sana kuvuta huduma ya maji kwenye majengo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha ajabu, gharama za uvutaji wa mabomba hayo kuingiza ndani ni kubwa. Kiwango cha chini ni kuanzia laki tatu mpaka laki nane na ni mita kama kumi tu lilipo bomba lile kuingiza ndani, mtu anachajiwa laki tatu; watu wa vijijini watapata wapi shilingi laki tatu kwa ajili ya kuvuta maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara ijaribu kuangalia gharama hizi waweze kupunguza ili wananchi walio wengi waliokuwa na hamu ya kutumia maji ya Ziwa Victoria waweze kuvuta maji waweze kuyatumia ndani ili waweze kufaidika na mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukamilika mradi huu wa vijiji 12, nina kata 15 na nina uhaba mkubwa sana wa maji kwenye jimbo langu. Je, Wizara ina mpango gani sasa wa kusambaza maji kwenye Kata zifuatazo; Nyugwa, Nyijundu, Busorwa, Kaboha, Shabaka, Nyang’hwale, Nundu, Mwingilo, Hafita na Nyabulanda? Maeneo yote yale yana uhaba wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa bahati nzuri mradi huu ulikuwa na thamani ya bilioni 15, kwa usimamizi mzuri wa Wizara chini ya Mheshimiwa Waziri Aweso, tumeweza kubakiza chenji zaidi ya bilioni tatu. Kwa nini hizo bilioni tatu zisiwekewe sasa utaratibu ulio mzuri kuanza kuweka utaratibu wa kuweza kupeleka baadhi ya hizo kata.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nakuomba, mradi huu ili tuweze kuufaidi mradi huu vizuri ninaomba sana Meneja wa RUWASA awe karibu na wananchi. Kwa sababu leo hii Meneja wetu wa RUWASA wanamtafuta wananchi ili waweze kwenda kufanyiwa tathmini ya kuvuta mabomba majumbani mwao, ile ofisi inakuwa wale watu hawapatikani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba Meneja wa RUWASA – ninamsifu kwa kazi yake nzuri – awapokee wananchi wangu, awaambie gharama na ikiwezekana awape muda maalum kwamba ukilipia leo hii baada ya siku fulani maji utayapata. Lakini majibu yamekuwa hayaeleweki, bei zinakuwa ni kubwa lakini hawapewi muda maalum wa kwamba utakapolipa ni muda gani utapata maji; naomba hili lichukuliwe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata asubuhi niliuliza kwenye swali la nyongeza, nilitoa ushauri kwamba kwa nini Wizara isiweke mfumo kama wa TANESCO kufunga mita za kutumia luku ili kupunguza hii sintofahamu na kutengeneza mazingira ya rushwa. Nitatoa mfano; leo hii Dar es Salaam, kila wanapopita wasomaji wa mita lazima kila mwezi nitume mtu wa kwenda kurekebisha. Unaambiwa 180,000 lakini akienda mtu kule kurekebisha anaambiwa kuna makosa ya kiuandishi tunapunguza gharama unalipa kiasi fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii Dar es Salaam tufanye mfano ina watumiaji wa maji labda 1,000, wasomaji wa mita wako watano, kwa nini wasifanye haya makosa? Lakini mtakapotumia huu mfumo ambao ni wa kufunga mita ambazo mtu anatumia kutokana na mahitaji yake, akiwa na shilingi 1,000 anunue 1,000 akiwa na 10,000 anunue 10,000 na akiwa hana inakata kuliko haya masuala ya kila mwisho wa mwezi wanapita wasomaji wa mita, wanakuwa wanachoka. Anakwenda chini ya mti anatafakari tu hii nyumba tuiandikie ngapi anaandika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli hili linafanyika na ni mhanga mmoja wapo. Huwa ninalipa bili ya shilingi 50,000 mpaka 60,000 lakini unakuta inaandikwa mpaka shilingi 200,000, ukituma mtu anakwenda kurekebishiwa; hii ni sehemu yangu moja, je ni watu wangapi ambao wanapata shida kama hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hii inajenga mazingira ya rushwa pia. Mtakapofunga hizi mita haya mazingira yaliyopo hayatakuwepo, hata zile foleni za watu kwenda pale kwenye Wizara ya Maji kurekebisha bili zao hazitakuwepo. Chukueni mfano huo upande wa TANESCO, leo hakuna foleni kwenye masuala ya ulipaji, mtu ananunua luku kulingana na uwezo wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naomba myachukue haya mawazo yangu myafanyie kazi, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Kwa sababu dakika tano ni chache, napenda niseme yaliyomo ndani ya moyo wangu, bajeti hii haikugusa kabisa maeneo ya Nyang’hwale hata sehemu moja. Kuna ahadi za Viongozi Wakuu kuanzia Mheshimiwa Rais Kikwete alikuja 2010 akatuahidi Barabara ya kutoka Kahama - Nyangh’wale kwenda Busisi itajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2013 Mheshimiwa Jakaya alikuja kwa mara nyingine akatuahidi vile vile. Mwaka 2015 mgombea mwenza ambaye sasa hivi ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan alikuja kwenye kampeni na akatuahidi kwamba barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami. Mwaka 2015, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwenye kampeni zake alipokuja, alituahidi ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha ajabu kuanzia mwaka 2010 mpaka leo hii 2021 haijawahi kuwekwa ndani ya mpango hata siku moja, hata bajeti hii nimeangalia hakuna mpango wowote ambao umewekwa ujenzi wa lami wa barabara hiyo. Wakati barabara hiyo inaunganisha Mikoa mitatu Shinyanga Geita na Mwanza. Barabara hiyo itafungua uchumi wa Nyang’hwale kwa sababu Daraja letu la kutoka Busisi - Kigongo Feri litakapokuwa liko tayari, kutoka Busisi kwenda Kahama ni kilometa chache sana kuliko kuzunguka Shinyanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nasema kama mwakilishi wa Jimbo la Nyang’hwale, kwa kweli sijaridhika, naomba bajeti hii tuwaondoshe hawa Mheshimiwa Waziri na timu yake ikajipange upya. Kwa sababu kila Mbunge amesimama hapa anamlalamikia Mheshimiwa Waziri na Wizara yake hakuna hata Mbunge mmoja aliyeridhishwa na bajeti hii. Kwa hiyo naomba nitoe hoja, Wabunge wenzangu mniunge mkono, Wizara hii iweze kuondoka wakajipange upya Wizara hii

Waheshimiwa Wabunge, naomba mniunge mkono. (Makofi)
NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tukae. Mheshimiwa Amar kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Gwajima.

MHE. ASK. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu nimpe taarifa ndugu yangu na rafiki yangu kwamba Urais siyo mtu Urais ni taasisi. Anapoahidi Rais imeahidi taasisi ya Urais, kwa hiyo namshauri kwamba kama vile mimi nilivyoahidiwa pale Wazo, Mheshimiwa Rais alipopita pale akaahidi bilioni tano kwa ajili ya mafuriko, naamini Taasisi ya Urais itayatimiza hayo kwa hiyo namtaarifu avute subira tutatimiziwa tu nampa taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Amar.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa yake Mheshimiwa siwezi kuipokea kwa sababu wananchi wangu hawatanielewa, niunge ama niache, ninachoomba ni kwamba mniunge mkono Wizara hii ikajipange upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, wamevunja kanuni.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, mmeeleweka. Mheshimiwa Amar malizia mchango wako. Ngoja kwanza Mheshimiwa Amar nifafanue jambo moja, maana, ngoja kidogo.

Waheshimwia Wabunge, naona mmesimama hapa kwa wingi baada ya kusikia neno Mheshimiwa Amar alikuwa anasema anataka kutoa hoja ili Bunge limtume Mheshimiwa Waziri akajipange upya ndo aje humu ndani. (Makofi)

Sasa Waheshimiwa Wabunge taratibu tulizojiwekea sisi wenyewe haziruhusu hiki ambacho anasema Mheshimiwa Amar. Kwa hiyo malizia mchango wako Mheshimiwa.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika…

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Charles Mwijage.

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji na wengine wote waliozungumza kama yeye, kwamba sisi Wabunge tunapaswa tunapochangia tumweleze Waziri na Serikali kwamba hizo pesa za barabara zote wakazipate wapi, kwamba Serikali sasa ingeamua iende ikope tujenge barabara halafu sisi tutalipa na watoto wetu hata kama ceiling itazidi. Naomba kumpa taarifa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, ndiyo maana nilimpa fursa amalizie muda wake mjadala anaousema Mheshimiwa Mwijage yuko sahihi, lakini siyo katika mjadala ngazi hii, siyo mjadala wa ngazi hii. Ngazi zinazofuata hapo baadaye Waheshimiwa Wabunge yale aliyoyasema Mheshimiwa Mwijage tutaweza kuyatumia huko mbele. Kwa hiyo tuanze kutafakari wale Wabunge ambao wanatamani mambo yabadilike kutokana na haya yaliyowekwa humu basi waanze kutafakari namna ya kuishauri Serikali ipate wapi hizo fedha, lakini siyo kwenye mjadala wa ngazi hii ambapo tunajadili bajeti za kisekta. Mheshimiwa Hussein Amar.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, hata wewe jana umelalamika sana jimboni kwako na wengine wote tunalalamika hivyo hivyo, lakini pia tukumbuke kwamba tunapowakusanya wananchi na kuwaeleza mipango ya Chama na Serikali itafanya nini mtakapotupa ridhaa, ni haya sasa ya kuwatengenezea yale ambayo tuliwaahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii mimi kama Mbunge mwakilishi, kazi za Mbunge ni tatu; kuishauri Serikali, kuisimamia Serikali pamoja na kutunga sheria. Sasa leo hii mimi kama mwakilishi wa Jimbo nakuja hapa nakaa naunga tu mkono wananielewaje mimi wale kule?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tuelewane vizuri, nitaruhusu hii taarifa lakini Mbunge atakayesimama kwenye taarifa asiwe anachangia kwamba na Jimboni kwangu kunafanana na wewe, awe anampa huyo taarifa juu ya kile anachokichangia.

Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa mchangiaji kwamba barabara hii ya Busisi - Nyang’hwale Kahama haina umuhimu tu kwenye Jimbo la Nyang’hwale isipokuwa ina umuhimu mkubwa sana katika Jimbo langu katika Kata ya Chela, Kata ya…

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hayo ndiyo niliyokuwa nayasema sasa, yaani Mbunge hujapata nafasi ya kuchangia unataka utumie kwenye taarifa kuchangia. Sasa kuanzia sasa hivi nitakuwa nawakata tu, Mheshimiwa Iddi kaa chini. Kuanzia sasa hivi ukisimama ukataka kuchangia unamkosea yule anayechangia kwa sababu kwenye Taarifa Rasmi za Bunge zitaonekana ulimpa taarifa halafu unazungumzia mambo ya kwako wewe, tafuteni fursa ya kuchangia Waheshimiwa Wabunge. Mheshimiwa Amar.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2010 nilipata kura nyingi sana na Chama na Kiongozi Mkuu wa nchi alipata kura nyingi sana. Mwaka 2015 hivyo hivyo, 2020 hivyo hivyo kwa imani kubwa ya kwamba tutawatengenezea barabara wananchi hawa. Mwaka 2025 nitaenda kusimama niseme nini, lakini pia Wabunge wote wamelalamika kwa nini wasitoke wakajipange upya?

Mheshimiwa Naibu Spika, hii si mara ya kwanza mimi ni awamu yangu ya tatu, tuliwahi kuiondosha Wizara ya Maji ikaenda ikajipanga upya, leo hawa vipi? Wabunge wote wamelalamika, mimi sina hata kilomita moja leo miaka 12, nitawaeleza nini wananchi. Naomba sasa kwamba Mheshimiwa Waziri safari hii sijui niunge mkono, sijui namna gani, lakini akajipange upya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri pamoja na Naibu Waziri wa Wizara hii; Katibu pamoja na watendaji wao wote kwa kazi nzuri ambazo wanaendelea kuzifanya. Pia napenda kuunga mkono hoja kutokana na hizo dakika tano kuwa ni chache sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba umeme ni maendeleo lakini pia ni huduma. Lengo la Serikali ni kusambaza umeme vijijini zikiwemo na taasisi za umma kama vile zahanati, vituo vya afya pamoja na shule za msingi na sekondari.

Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo langu la Nyang’hwale nina vijiji 62, vijiji ambavyo tayari vimeshapitiwa na umeme mpaka sasa hivi ni vijiji 44 bado vijiji 18. Katika vijiji 44, nakuomba Mheshimiwa Waziri ongea na Waziri wa TAMISEMI ili sasa Wakurugenzi waweze kupewa maelekezo wa nchi nzima wakiwemo wa Nyang’hwale ili waweze kulipia zile gharama za Sh.27,000 ili taasisi zetu; zahanati, shule za msingi na sekondari ziweze kulipiwa na kupewa huduma ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la pili kwamba Wilaya ya Nyang’hwale ina wachimbaji lakini pia umeme tunauhitaji sana kwenye maeneo ya wachimbaji. Maeneo hayo ni kama vile Igalula, Isekeli, Ifugale na maeneo mengine, waweze kuvutiwa umeme kule ili waweze kuendesha shughuli zao kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, shida kubwa iliyoko jimboni na maeneo mengine wamezungumza Waheshimiwa Wabunge, jambo la kukatikakatika kwa umeme linawatia hasara sana wananchi. Umeme kwa Jimbo la Nyang’hwale unakatika zaidi ya mara tatu au nne kutwa nzima. Vifaa vya umeme vinaharibika lakini pia bidhaa zilizomo ndani ya freezer, vinaharibika. Tatizo ni nini? Kwa sababu umeme unakatika unatutia hasara sana wananchi hasa tunaotumia umeme kwenye majumba yetu na shughuli zetu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimepewa jina la mkandarasi wangu atakayeenda kusambaza umeme katika vile vijiji 18. Cha kushangaza na kusikitisha ni kwamba nimeongea naye jana akasema mpaka sasa hivi hajapata fedha kutoka CRDB, tatizo ni nini? Mheshimiwa Waziri lichukue jambo hili ongea naye kujua kwa nini hajapewa fedha mpaka sasa hivi ili aweze kwenda site. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, gharama ya kuunganishiwa umeme ni Sh.27,000, lakini wananchi wetu wapo maeneo mbalimbali, unakuta kutoka eneo moja kwenda eneo lingine ni zaidi ya mita 500 mpaka mita 1000, je, huyu aliyeko kwenye mita 500 mpaka mita 1000 gharama ni hiyohiyo Sh.27,000, nguzo na nyaya hazimhusu? Kwa hiyo, pamekuwa na changamoto nyingi, kuna wananchi wetu wengine wamelipia muda sana zaidi ya miezi mitano mpaka mwaka mmoja hajavutiwa umeme anaambiwa tatizo ni nguzo, hasa tuambieni Sh.27,000 ukiwa ndani ya mita ngapi unafungiwa umeme kwa haraka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli mimi sina mchango mkubwa zaidi yangu ni hayo, lakini nampongeza sana Mheshimwia Waziri kwa kazi nzuri na Naibu Waziri na Katibu kazi zao ni nzuri na wanachapa kazi. Mheshimiwa Waziri yachukue haya ambayo nimeyachangia kwenye upande wa Jimbo langu la Nyang’wale.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi hii niweze kuchangia. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kunipa kibali cha kuweza kusimama hapa leo nikiwa na afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu wake kwa hotuba nzuri sana ya mwelekeo wa mwongozo wa mpango wa mwaka 2022/2023. Lakini pia nikupongeze wewe na Naibu Spika kwa kazi nzuri ambazo mnaendelea kuzisimamia katika Bunge hili ambalo kwa kweli unaliendesha kwa kiwango cha hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kuungana na Wabunge wenzangu kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu, Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri ambazo anaendelea kulitumikia Taifa letu bila kujali tofauti zetu za kisiasa, udini, kanda, ukabila, na wote tunashuhudia; mama kazi iendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameweza kushusha fedha nyingi sana katika miradi ya maendeleo kwa nchi yetu, miradi ya afya, elimu, maji n.k. lakini pia kwa Wilaya yangu ya Nyang’hwale kwa kweli Mheshimiwa Rais ameweza kutumwagia fedha nyingi kwa kipindi kifupi, zaidi ya bilioni nane kwenye miradi mbalimbali ya afya, elimu, maji, miundombinu hadi TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni mfupi sana kwa leo, ushauri wangu Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, nizungumzie upande wa sekta ya madini; sekta hii hivi sasa na yenyewe inachangia sana pato la Taifa. Lakini pamoja na uchangiaji wa pato kubwa la Taifa kutokana na madini hizo fedha ambazo zinapatikana kwa wachimbaji wadogo ni fedha ambazo tunaona ni nyingi sana, lakini nasema ni kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana katika mpango huu tuweke mkakati wa kuweza kuwawezesha wachimbaji wetu wadogo ili waweze kuweza kujipatia kipato na kuongeza kipato cha Taifa. Leo hii tunasema sekta ya madini imechangia zaidi ya bilioni 500, ni wachimbaji wanaotumia sululu, je tukiwawezesha wachimbaji hao tutakusanya mabilioni na tutapata mabilioni mengi kutokana na hawa wachimbaji wetu wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapohapo kwenye upande wa sekta ya madini, Mheshimiwa Waziri ninaomba sana sasa hivi kumekuwa na utoroshwaji mkubwa sana wa dhahabu inayotokana na uchenjuaji wa kutumia mercury. Kwa hiyo ninaomba sana tuweke mikakati madhubuti ya kuweza kuitambua ile mialo na kuwatambua hawa wachennjuaji wanaotumia mercury ili tuweze kuidhibiti dhahabu hiyo ambayo sasa hivi inatoroshwa kwa wingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo bilioni 500 ambazo tumezipata zinatokana na wale ambao wana elution machine na wale ambao wana VAT leaching. Lakini kwa hawa wachenjuaji wadogo kwa kweli dhahabu zao hazukusanywi ipasavyo, kwa hiyo Taifa linapoteza mapato sana. kwa hiyo kwenye mpango wetu huu wa 2022/2023 tuweke mkakati ulio mzuri zaidi tuweze kuwatambua hao wenye mialo ili tuweze kuzikusanya hizo dhahabu tuweze kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, naomba pia nizungumzie kuhusu TRA; ushauri wangu, kwa kweli naiomba Serikali kupitia TRA waweze kuongezewa kibali cha kuajiri watumishi ili waweze kuwa wengi, waweze kudhibiti huu mtindo uliopo sasa hivi ambao wafanyabiashara wanakwepa sana kutoa risiti kwa sababu watumishi wa sekta hiyo ya TRA wanakuwa ni wachache, hawapiti maeneo mbalimbali kufanya ukaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalisema ushahidi wake ninao. Kwa sababu unapoingia dukani mpaka sasa hivi bado kuna mtindo wa wafanyabiashara anakuuliza nikupe bei ya risiti ya mkono ama ya EFD machine. Kwa nini wanasema hivyo; ni kwa sababu usimamizi haupo wa kutosha. Kwa hiyo, ninaomba sana TRA wajaribu kuangalia upande huo. Bado Serikali inapoteza mapato makubwa sana kwa wafanyabiashara wetu kwa sababu bado wanakwepa kutoa risiti za EFD machine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ushauri mwingine kuhusu suala hilo la TRA. TRA izidi kabisa kuendelea kutoa elimu ya mlipakodi, lakini pia kwa waanyabiashara wetu pamoja na wanunuzi. Elimu hii bado inahitajika sana, kwa sababu leo unakuta mtu anaulizwa nikupe risiti ambayo ni ya mkono au ya EFD machine, anapewa bei mbili tofauti kwa sababu elimu hiyo haijawafikia vizuri sana Watanzania walio wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, natoa ushauri kwamba tuweke mikakati ya kutosha kuhusu hawa wao wafanyabiashara wanaokwepa, ama kuwaongezea adhabu. Lakini pia wanunuzi wanaonunua bila kuomba risiti atakapokamatwa na kifaa ama bidhaa ambayo haina risiti inabidi naye adhibitiwe na afikishwe sehemu husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani? Sisi Wabunge tuliomo humu, kwa ushahidi ninao kabisa, tunakutana maeneo mbalimbali iwe kwenye maduka ama kwenye huduma mbalimbali, huwezi ukamkuta Mbunge anaomba risiti, wakati ni kiongozi. Kwa hiyo, na sisi Wabunge hebu tuwe sasa mstari wa mbele kuanza kuomba risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili uthibitisho ninao. Nikiwauliza hapa Waheshimiwa Wabunge tunaoingia kwenye migahawa wangapi tunatoka na risiti? Tunaoingia kunyoa vipara ama kutengeneza saluni ya akinamama, akina mama wangapi Waheshimiwa Wabunge wanatoka na risiti za saluni, wangapi? Kwa hiyo, nasema hayo kwa sababu nina ushahidi na tunakutana maeneo hayo mbalimbali, na sisi pia kama viongozi tuwe mfano wa kuweza kukusanya kodi kwa ajili ya pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kidogo kwenye huu mpango. Kwanza kabisa nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu, ambaye ameniwezesha kunipa afya njema na kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyotoa mwongozo kwamba unaweza ukasema ametangulia kusema Mheshimiwa Muhongo profesa, Mheshimiwa Kimei na mimi hapa darasa la saba naomba nitoe mchango wangu, pamoja na kwamba wamenitangulia hawa vigogo. Mpango huu kwanza nianze kumpongeza Waziri wa Fedha kwa Mpango mzuri ambao ameuweka hapa mbele tuweze kuujadili. Nitakuwa na yangu machache sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kama atakumbuka huwa nalalamika kila mara, kila Bunge linapofikia kipindi kama hiki kwa kumwambia kwamba upotevu wa fedha kwenye maeneo mbalimbali ni upotevu mkubwa sana ikiwa kwenye maeneo hususani kwa wafanyabiashara. Hili pato ambalo tunalizungumzia limekua, lingeweza kukua zaidi iwapo tutaendelea kusimamia vizuri ukusanyaji wa mapato kwenye maeneo yetu ya watu wanaofanya biashara. TRA ina upungufu kidogo pamoja na kwamba inafanya kazi vizuri, lakini kuna wafanyakazi au watumishi wa (TRA) ambao siyo waaminifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano kwenye Jiji la Dar-es-Salaam kwa sababu naishi hapo, ukweli ukizunguka kwenye maeneo mbalimbali ya wafanyabiashara, hususani kwenye maduka unakuta watu wengi wananunua bidhaa na hawapewi risiti. Hili lipo kwa asilimia mia moja linafanyika, kama wanatoa risiti basi ni kwa asilimia kumi ama kumi na tano na hao wanaotoa risiti, umenunua mali ya shilingi milioni moja, unapewa risiti ya shilingi laki moja. Hawa wafanyabiashara wanapata wapi hicho kiburi? Mheshimiwa Waziri wa Fedha, naomba hili ulichukue ukae na hicho kitengo cha (TRA) wajaribu kuangalia huu upungufu watauzuia vipi, kwa sababu leo hii tuna mambo mengi ambayo tunahitaji yakafanywe kwenye maeneo yetu. Kama fedha haitakusanywa vizuri, haya maeneo yatafanyiwa vipi kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna maeneo mengine ambayo inabidi tuyaangalie. Kuna watu wanahitaji kulipa fedha za Serikali kupitia control number, unakuta mtu anafuatilia siku tatu nne mpaka wiki hajapewa control number, je, hiyo fedha aliyonayo mfukoni haitapata kazi nyingine? Suala hili nalo wajaribu kuliangalia sana kwa sababu watu wanaenda kuomba kulipa fedha ya Serikali, kuna tatizo gani kumpa siku hiyo hiyo control number? Inachukua mpaka wiki nzima, control number haijatolewa. Huu nao ni upungufu na unasababisha kupunguza mapato ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia mpango wa Serikali, namna gani tuboreshe tuweze kukusanya pato la Taifa. Nizungumzie upande wa madini, wachimbaji wetu wa madini hivi sasa wanaongeza ama wanachangia pato la Taifa kutoka asilimia nne mpaka asilimia nane. Hata hivyo, watu hawa wachimbaji wetu ama sekta hii ya madini ikiwaboreshea vizuri wachimbaji kwa kweli Wizara hii ya Madini inaweza ikachangia pato la Taifa hata zaidi ya asilimia ishirini. Nitatoa mfano kidogo, wakiwezeshwa hawa wachimbaji wetu, mfano, STAMICO anafanya utafiti wa kufanya explorations ili kujua huyu mchimbaji anapata wapi madini na kwa kiasi gani ili aweze kupata mapato makubwa. STAMICO ama hawa GST wanafanya gharama zao kuwa ni kubwa sana, kiasi kwamba, hawa wachimbaji wadogo ama wachimbaji wa kati wanashindwa kumudu gharama za kufanyia explorations, matokeo yake wanakwenda kufanya uchimbaji ambao ni local. Kwa hiyo mapato hayapatikani kwa wingi, lakini wakiwezeshwa kwa kupunguziwa gharama za kufanyia explorations na pia kuwezeshwa vyombo vya kiuchimbaji vya kisasa, naamini kabisa Wizara ya Madini inaweza ikaongeza pato lake katika Mfuko wa Taifa kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kukusanya mapato hayo, tunahitaji tufanyiwe mambo mengi. Hata hivyo tuangalie kwenye upande wa sekta ya kilimo, leo hii mvua zetu zimekuwa ni za rasharasha, lakini kilimo kinachangia kipato kikubwa sana. Leo hii katika maeneo mbalimbali tumekuwa na ukame, lakini mvua zinaponyesha kuna maji mengi yanapotea, kwa nini Serikali ama Wizara ya Kilimo isiweke mkakati mzuri wa kuweza kujenga mabwawa makubwa ili sasa kipindi chote cha mwaka kiwe ni kipindi cha kulima. Wakulima watakapopata mazao ina maana tunanyanyua pato letu la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano kidogo, kwenye maeneo kama vile Jimbo la Nyang’hwale. Jimbo la Nyang’hwale tuna maeneo mengi sana ya mabonde ambayo maji yanatiririka yanakwenda Ziwa Victoria. Yale maji yangeweza kutegwa na kuweza kumwagilia na kupata mazao, tungeweza kuchangia pato. Hilo ni eneo moja, je, ikiwa kwa nchi nzima? Kwa hiyo naomba hili nalo lichukuliwe liwe katika vyanzo vyetu vya mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyanzo vyetu vya mapato tukivipata, basi Serikali isisahau basi kuweka mpango wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Busisi - Nyang’hwale kwenda Kahama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanyia nchi hii. Lakini pia nimpongeze Waziri wa Madini Mheshimiwa Doto Biteko pamoja na timu yote.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo, kutokana na muda nataka nitoe ushauri kidogo kwenye Wizara hii, ushauri wangu wa kwanza ni pamoja na kwamba plants nyingi nchini zinaliingizia Pato la Taifa, plants nyingi za VAT reaching zinalipatia Taifa mapato makubwa sana; ikiwemo Nyangh’wale ambayo tuna plant zaidi ya 100. Uchenjuaji huu una sababisha uharibifu wa mazingira. Ushauri wangu kwamba plant zote nchini ikiwemo na plant za Nyangh’wale Serikali ielekeze kwamba kila plant ipande miti zaidi ya 200 ili kuepusha majanga ya uharibifu wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa pili Mheshimiwa Waziri Doto Biteko, uunde tume ili iweze kwenda kwenye mgodi wetu wa Bulyanhulu kufanya uchunguzi wa uchimbaji unaoendelea kule chini. Inasemekana kwamba uchimbaji huu umeelekea zaidi kwenye upande wa Nyangh’wale na siyo Kahama. Watakapobaini kwamba ni kweli uchimbaji huu unaelekea Wilaya ya Nyangh’wale basi tukae chini ili tuweze kurekebisha ushuru ambao tulikuwa tukipata. Kutoka kwenye asilimia 100 Msalala walikuwa wakipata 67 na Nyangh’wale tulikuwa tunapata asilimia 33. Iwapo sasa hivi uelekeo huo utakuwa unaelekea Wilaya ya Nyang’wale itabidi tubadilishe. kwamba sisi tuchukue 67 na Msalala wachukue asilimia 33.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu mwingine ni kwamba, Wizara imeruhusu uchimbaji unaoitwa uchimbaji wa rash maeneo mbalimbali nchini. Sasa kwenye uchimbaji huu wa rash pamejitokeza vikundi ambavyo vinasimamia kukusanya mapato yanayopatikana pale. Kumejitokeza pia vijana ama wananchi fulani wachimbaji wanaojiita wababe wachimbaji ambao wamekuwa wakizivamia zile ofisi za rash ambazo zinakusanya mrahaba wa mawe. Kwa mfano kikundi cha akina mama wachimbaji wadogo wadogo wa Nyangh’wale walivamiwa na kufanyiwa usumbufu mkubwa sana na vijana hawa. Kwa sababu Serikali imeruhusu ofisi hizi zisimamie rash, ninakuomba Mheshimiwa Waziri utoe tamko utundu huo na ujeuri huo unaofanywa na hao vijana uachwe kabisa.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nashukuru kwamba hawa akina mama baada ya kuvamiwa namshukuru sana DC wangu pamoja na RMO wamelishughulikia jambo hili na limekaa vizuri wale akinamama wanaendelea na shughuli zao. Hongera sana Mheshimiwa DC kwa kulimaliza tatizo hili. Mheshimiwa Spika, ushauri wangu mwingine, ni kwamba kuna wachimbaji ambao wanapeleka carbon zao kutoka Nyangh’wale kwenda kuchomea Geita mji carbon hizo zinapochomwa Geita na dhahabu inapopatikana, imekuwa kodi zote zinachukuliwa na Geita mji ikiwa mrahaba wa Serikali lakini pia service levy, Wilaya ya Nyangh’wale tunakuwa hatupati service levy kwa sababu wametoka Nyang’wale wameenda kuchomea carbon zao Geita. Takriban zaidi ya milioni 800 zimeng’ang’aniwa na Mji wa Geita. Tunakuomba Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko lisimamie hili ili tuweze kurudishiwa hizo milioni 800 ziweze kuleta maendeleo katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Nyang’wale.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Doto Waziri wa Madini, mwisho kabisa, pesa hizi zimekuwa zikiombwa na zimeleta mgogoro sana. Ni kwanini wanaenda kuchomea Geita? Ni kwa sababu wale wachimbaji wanakuwa hawana uwezo wa kuendesha shughuli zao, wanakwenda kukopa kwa wale matajiri walioko Geita, sasa badala ya kuchomea mzigo huu Wilayani Nyangh’wale, wanabeba ule mzigo kuupeleka Geita wanapochomea. Geita kule kwa wale matajiri wanalipa zile…

SPIKA: Mheshimiwa Hussein Amar kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kanyasu.

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, namheshimu sana Mheshimiwa Hussein na natambua mchango wake. Lakini, kwa mujibu wa sheria ya service levy inalipwa pale ambapo mfanyabiashara anafanyia biashara yake na kwamba Halmashauri ya Mji wamekuwa wakitoza hivyo kwa sababu sisi hatukuwafata Nyangh’wale wanakuja wenyewe nakushukuru sana.

SPIKA: Mheshimiwa Hussein Amar unapokea taarifa hiyo?

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, taarifa hii siipokei. Namheshimu sana mdogo wangu Kanyasu. Wale wanapochukua carbon zao Wilayani Nyangh’wale kwenda kuchomea Geita ni kwa sababu wanapewa mikopo na wale matajiri waliopo Geita. Lakini kwa sababu address ni kwamba ametoka Nyangh’wale tunaomba ile service levy irudi kwetu Nyangh’wale vinginevyo Mheshimiwa Waziri basi uweke zuio la watu kubeba carbon kutoka Nyangh’wale ziende Geita zisiende Geita hizo carbon kwa hiyo tunaomba utusaidie hilo; kwa sababu wachenjuaji wengi wanapeleka Geita kwa sababu wanaenda kukopa kule. Iwapo Mheshimiwa anasema kwamba ni sheria basi hebu kuiangalia hii sheria, tuweke zuio ili carbon isitoke Nyangh’wale ichomewe pale pale Nyangh’wale na isiende Geita.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia Wizara hii ya Maji. Lakini kwanza kabisa nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kunipa afya njema na kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji Nyamtukuza Bukwimba. Mradi ule kwa kweli ulikuwa ni mradi ambao Mheshimiwa Waziri wa Maji anasema kichefuchefu. Lakini mradi ule ulikuwa ni kichefuchefu zaidi kwa sababu mradi ule ni tangu 2014 tuliuanza kutekeleza lakini kulitokea mambo mbalimbali ambayo yaliwasababisha baadhi ya Mawaziri kuja kuutembelea mradi ule. Naomba niwataje wale Mawaziri waliokuja kuutembelea mradi ule ambao ulikuwa na matatizo makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo uliweza kutembelewa na Waziri wa kipindi kile Profesa Mbalawa alifika kwenye mradi ule lakini pia Injinia Kamwelwe na yeye alifika kwenye mradi ule. Lakini pia Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa na yeye alifika kwenye mradi ule. Lakini pia Waziri wa sasa wa Maji Aweso pia amefika kwenye mradi ule pamoja na Naibu wake Waziri amefika kwenye mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, mradi ule uliweza kutembelewa na Katibu Mkuu, Wizara ya Maji wa kipindi kile Kitlya Mkumbo naye alifika. Lakini Katibu Mkuu wa sasa naye alifika kwenye mradi huo wa maji wa Injinia Sanga. Kwa kweli nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ulipofika kwenye ule mradi kwa kweli ulitoa maagizo makali na mradi ule ukaanza kwenda. Lakini alivyokuja Waziri Aweso yeye ndiye alikuja na moto mkali, aliwatia pingu baadhi ya Makandarasi na mradi ule ukaenda speed. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, Naibu Waziri na yeye alikuja na moto mkali kwa kweli tunashukuru mradi ule mpaka sasa hivi umeanza kutoa maji. Wananchi wa Nyang’hwale wanaipongeza sana Serikali lakini pia wanakupongeza sana Mheshimiwa Waziri Aweso pamoja na Naibu wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna vitu nataka niviseme. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha nyingi kwenye miradi mbalimbali ikiwemo mradi wa maji wa Nyang’hwale. Lakini pia nizidi kumpongeza Waziri wa Maji rafiki yangu Juma Aweso pamoja na Naibu Waziri wake Prisca Mahundi pamoja na Katibu Mkuu Sanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu umeenda kukamilika lakini nizidi kuipongeza Serikali kwa kuendelea kukamilisha miradi mikubwa nchini ikiwemo mradi huo wa Nyamtukuza, Nyang’wale lakini pia Bukwimba. Mradi huu kwa bahati mbaya umekuwa na maji ambayo si mazuri kwa matumizi ya binadamu. Mradi huu umeenda kukamilika, hauna chujio la maji. Mpaka sasa hivi wananchi walio wengi wanaogopa kuunganisha maji na kuyatumia maji yale kwa sababu yanaweza kuharibu afya zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaiomba Serikali Mwaka wa Fedha 2022 tuliweza kutengewa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa mradi 2,400,072,000/= lakini fedha hizo tumeweza kupokea bilioni mbili peke yake. Ina maana kuna upungufu ambao hatukupata hizo pesa karibu milioni miatatu naa. Na Mwaka huu tumetengewa 2,098,000,000/= kwenye Bajeti hii ambayo tunaenda kuipitisha hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu sikivu iweze kuzitoa fedha zote hizo ili tuweze kukamilisha mradi huo ikiwemo kujenga chujio la maji kwa sababu ndiyo kipaumbele chetu. Lakini cha ajabu nimeweza kuangalia kwenye kabrasha tenki letu lile limeshafanyiwa usanifu. Tenki la uchujaji wa maji ambalo litagharimu bilioni 1.8. Lakini Wizara mmetutengea milioni 220. Huu mradi wa kujenga hilo chujio utakamilika lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wananchi wanamatumaini makubwa sana, Mheshimiwa Aweso kwamba utatupa hiyo bilioni 1.8 tuweze kujenga hilo chujio la maji ili tuweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nikwambie ukweli, mradi ule tumeusubiri kwa muda mrefu sana tangu mwaka 1975 wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale hawajawahi kunywa maji ya bomba. Kwa hiyo, matumaini yao ni makubwa sana kwamba sasa hivi mradi huu utaenda kukamilika. Tutaweza kuyasambaza maji haya kwenye Kata zifuatazo; Kata ya Nyamtukuza, Kata ya Kakola, Kata ya Nyugwa, Kata ya Karumwa, Kata ya Kafita, Kata ya Nundu, Kata ya Bukwimba, Kata ya Busorwa, Kata ya Kaboha, Kata ya Nyang’wale, Kata ya Shabaka, Kata ya Izunya, Kata ya Nyabulanda, Kata ya Mwingilo, Kata ya Nyijundu na Vijiji vyake. Tuna matumaini makubwa sana ya mradi huu kupunguza kero ya maji ya tangu mwaka 1975. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe Wizara ya Maji kuhusu mradi mkubwa ambao unatekelezwa kutoka Mangu kwenda Ilogi. Mradi wa pamoja kati ya Serikali na Mgodi wa Bulyang’uru. Mradi ule tayari umekamilika, naiomba Wizara sasa iruhusu maji haya yaanze kutumika kwenye Vijiji vifuatavyo. Maji haya yako tayari kutumiwa lakini tunashangaa kwa nini Wizara haijatoa kibali ili maji yale yaanze kutumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuomba Mheshimiwa Waziri Aweso toa kibali ili maji haya wananchi waanze kuyatumia kwa sababu maji haya ni safi na salama ambayo yanatoka Ihelele kwenda Shinyanga. Maji haya yanapita kwenye Kijiji kifuatacho; yanapita Ngushimba, yanapita Nyugwa, yanapita Mwamakiligwa, yanapita Kafita na Lushimba. Toa kibali ili wananchi hawa waanze kunufaika na haya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri naamini kabisa utendaji kazi wako na uchungu ulionao, kibali hiki hutachelewa kukitoa, Viongozi wengine wote walioko hapa wa Wizara ninaamini wamenisikia kilio cha wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale lakini mradi huu wa Ilogi-Mangu upewe kibali ili wananchi waweze kuyatumia maji haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nitumie nafasi hii ya kuwapongeza Mameneja wafuatao; kwanza Meneja wa Mkoa wa Geita, Injinia Jabir lakini pia Meneja wa Wilaya ya Nyang’hwale Injinia Moses. Ukweli watu hawa tunashirikiana nao vizuri sana, kama Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale pamoja na Wabunge wa Mkoa wa Geita tunaamini na tunawaamini kazi zao wanachapa kazi. Kama kuna promotion zaidi ya hapo basi jaribuni kuwaangalia. Lakini tunaomba wabaki pale angalau hata kama ni miaka mitano sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nadhani kilio changu leo kikubwa ilikuwa ni chujio la maji. Zitolewe hizo bilioni 1.8 na zitolewe hizo bilioni 2 tuweze kusambaza maji kwenye Kata ambazo nimezitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa uhai na afya njema kwa siku ya leo na kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha nyingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya afya na elimu. Sisi kama Wilaya ya Nyang’wale kwa fedha hizo ambazo mama ameweza kuzitoa kwa nchi nzima; na sisi kama Nyang’wale kwa mwaka 2022/2023 ametupatia zaidi ya shilingi bilioni 5.5 kwa ajili ya miradi ya maendeleo upande wa afya na elimu. Hongera sana mama, kwa kweli unafanya kazi kubwa, hongera sana, sisi tuko nyuma yako, kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya. Naipongeza Serikali kwa kuendelea kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nyang’wale. Pia namwomba Mheshimiwa Waziri atenge fedha kwa ajili ya kukamilisha jengo la Mkurugenzi wa Wilaya ya Nyang’wale ambaye hivi sasa anatumia jengo la Hospitali ya Wilaya na kumfanya DMO asiingie kwenye lile jengo. Kwa hiyo, tenga fedha ili ulikamilishe jengo la Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nyang’wale aweze kuhama aende kwenye jengo lake, na kumpisha DMO naye aingie kwenye jengo lake la utawala ili aweze kufanya kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilizopo kwenye sekta ya afya hususan kwenye Hospitali ya Wilaya ya Nyang’wale, Vituo vya Afya na Zahanati, kwa kweli kuna uhaba mkubwa wa watumishi. Uhitaji wa watumishi ambao wanahitajika katika Wilaya ya Nyang’wale ni watumishi 841, lakini waliopo hivi sasa ni 193, sawasawa na asilimia 22. Kwa hiyo upungufu ukiuangalia hapo, ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwa mwaka huu wa fedha basi tupatiwe angalau hata watumishi 100 ili tuweze kupunguza gap lililopo pale. Kwa sababu ukiangalia 842 na 193 ni upungufu mkubwa sana. Waliopo kwa kweli wamechoka, lakini nawapongeza sana wanajituma na wanafanya kazi kwa moyo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zipo. Kuna wananchi walijitolea kujenga maboma ya Zahanati na maboma ya Vituo vya Afya, wametoa nguvu zao. Namwomba Mheshimiwa Waziri kupitia bajeti hii atenge fedha ili kwenda kuziunga mkono juhudi za wananchi wangu waliojitolea kwa ajili ya kujenga maboma ya zahanati pamoja na Vituo vya Afya ili kuwatia moyo, ili kwa mara nyingine hata ukiwaambia njooni tuungane pamoja watakuwa wako tayari kuliko hivi sasa wanatoa nguvu zao lakini Serikali haiwaungi mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya elimu, naipongeza sana Serikali. Kwa kweli Mama amefanya kazi kubwa kwa kipindi hiki kifupi, tumeweza kujenga madarasa mengi upande wa sekondari, madarasa mengi shule za msingi na pia kwa shule shikizi. Tumeweza kufungua sekondari tatu mwaka huu wa fedha. Kwa kweli tunampongeza Mama, anafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, palipo na mafanikio hapakosi kuwa na changamoto. Namwomba Mheshimiwa Waziri wetu aweze kutenga fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za Walimu kwa sababu kuna upungufu mkubwa, lakini pia atenge fedha kwa ajili ya kumalizia maboma ya vyumba vya madarasa ili kuwaunga mkono wananchi ambao walijitolea katika ujenzi huo wa maboma ya madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna upungufu mkubwa upande wa sekta ya elimu. Tuna upungufu wa walimu takribani asilimia 70 katika Wilaya ya Nyang’hwale. Ukweli Mheshimiwa Waziri jaribu kuangalia sana upungufu huo na hususan kwenye elimu ya sayansi na hisabati walimu ni wachache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa ushauri, naomba unisikilize vizuri. Ushauri huu jaribuni kuufanyia kazi. Naomba myafanyie uchunguzi magenge ya vyakula vinavyouzwa nje ya mageti ya shule zetu za sekondari na msingi. Vyakula vile na vinywaji siyo salama sana kwa watoto wetu. Pia ukiangalia maeneo haya, tayari kuna viashiria; mimi ni mmoja wa waathirika katika watoto wangu ama katika familia yangu, ameathirika na vinywaji hivi vya hapo shuleni, sasa hivi ni teja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, angalieni sana usalama wa chakula na vinywaji vya watoto kwenye magenge yaliyoko nje ya mashule. Jaribuni kufanya utafiti kwa kuwa pia ni vyanzo vya kuanza kufundisha watoto wetu mambo machafu kutokana na hizo Shilingi elfu moja moja na mia tano tano ambazo tunawa. Ukifika muda wa kwenda kula, kanunue pipi, kanunue mandazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nakumbuka, Mzee Mkuchika anakumbuka, sisi tuliokuwepo zamani kidogo, tulikuwa tunafungiwa viazi, mihogo au mandazi, tunaondoka navyo nyumbani. Leo hii sisi tunaona watoto wetu ni bora umpe shilingi 1,000 aende akale chakula pale shuleni na chakula hicho kina madhara makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jaribuni kuchukua hata watoto kumi, mkawapime afya zao, utakuta watoto wanane wana matatizo kutokana na vyakula hivyo. Kama siyo Typhoid na maradhi mengine kutokana na hivyo vyakula. Hatujui vinatengenezwa kwa mfumo gani na nia zao ni zipi kutokana na hali iliyopo. Mheshimiwa Waziri chukua ushauri wangu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza TARURA, imefanya kazi vizuri sana katika Wilaya yangu ya Nyang’hwale. Mwaka huu wa fedha tunaoenda kuumalizia, 2022/2023 tumeweza kupokea zaidi ya shilingi bilioni 2.2. Pamoja na hayo, bado kuna matatizo kwenye Kata zetu. Naishauri Serikali iiongezee fedha TARURA ili aweze kufanya kazi vizuri kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kuna daraja ambalo linaunganisha kati ya Kata ya Kharumwa na Nyijundu, ni kilomita saba tu kati ya hizo Kata, lakini daraja hilo tumeshindwa kulijenga kwa sababu linahitaji fedha zaidi ya shilingi milioni 500. Nakuomba zitengwe Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kulijenga hilo daraja, barabara ile ifunguke. Kwa sababu barabara hiyo sasa hivi haitumiki, utakapotoka Kharumwa kwenda Nyijundu ni kilometa 30 kwa njia ya mzunguko, lakini ukitoka Kharumwa kwenda Nyijundu kwa njia ya mkato ni kilomita saba. Kwa hiyo, itasaidia sana kuinua uchumi wa wa Nyang’hwale, lakini kwa sababu tumejenga Hospitali ya Wilaya, ni karibu sana kuleta wagonjwa kwa njia ya mkato, kutoa wagonjwa wilayani na kupeleka Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili kwa ajili ya kutuongezea fedha tuweze kujenga hilo daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia Hoja iliyoko mbele yetu ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kunipa uhai na afya njema kwa siku ya leo kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuunga mkono hoja hii iliyoko mbele yetu. Ni hoja nzuri na nilikuwa nimejipanga vizuri sana kuweza kuchangia lakini kwa bahati nzuri hoja hii kwa kweli imenifilisi kwa kiasi kikubwa, lakini nitaendelea kutoa ushauri kwa sababu nilikuwa nimejipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Waziri wa Madini, Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko, pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Katibu wa Wizara pamoja na timu yote kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kuifanya katika Wizara hii; hongera sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo yangu ni machache sana; kuipongeza na kuishauri Serikali kupitia hii Wizara ya Madini. Nianze kwanza kwa kuwapongeza wachimbaji wadogo ambao wanaendelea kuchangia pato la Taifa kwa kiwango kikubwa, kwa asilimia 40, kwa dhahabu yote ambayo inapatikana Nchini Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasemi wanasema unapotaka kumkamua ng’ombe ili akutolee maziwa mengi ni vyema ukamnenepesha. Kwa nini nasema hivyo; nizishukuru taasisi za kifedha kwa kuendelea kutoa mikopo kwa wachimbaji wadogo, lakini naomba iendelee kutoa zaidi na kupunguza masharti kwa wachimbaji wetu wadogo ili waweze kupata vifaa vya kisasa waweze kuzalisha dhahabu kwa wingi na kuweza kuzidi asilimia ambayo sasa hivi wanachangia, asilimia 40. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa vichache sana kwa hawa wachimbaji wadogo ambavyo vinahitajika ni kama vile compressor, crusher, bombing, winch, digger, vilipuzi na vifaa vingine. Vifaa hivi wakiweza kukopeshwa wachimbaji wetu wadogo wakaondoka kwenye uchimbaji duni uliopo hivi sasa wa kutumia kushusha ama kupandisha mawe kutoka chini kwa kutumia roller ama kuingia ndani kwa kutumia mock wanaita ukweli uzalishaji utakuwa ni mkubwa na mapato yao yatakuwa makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba Wizara izidi kuzishawishi taasisi za kibenki ziweze kupunguza masharti ili kuwasaidia wachimbaji wetu wadogo waweze na wao kunufaika na mali hii iliyoko chini ambayo ni aina ya dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mchimbaji mdogo ninaomba Wizara hii iweze kuwasaidia wachimbaji wadogo, hususan wenye leseni kupitia GST waweze kuchimba maeneo ambayo yameshafanyiwa utafiti. Lakini pia GST ipunguze gharama zake za kuwafanyia utafiti hawa wachimbaji kutoka kwenye gharama ya shilingi 432,000 kwa mita na waweze kushusha angalau ifike hata shilingi 200,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakifanya hivyo watakuwa wamewasaidia sana hawa wachimbaji wadogo, pamoja na kwamba mnawakopesha wanakwenda kuchimba kwa kutumia ramli mafanikio hayatakuwepo. Lakini GST mkiwapunguzia hawa wachimbaji gharama za uchorongaji na mkaingia nao makubaliano, hata kama kwa malipo kidogo kidogo, watakuwa wanaifanya kazi kwa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nadhani unanisikia, nakuomba ulichukue hili. Washauri sana GST waweze kupunguza gharama za utafiti za uchorongaji ili wananchi wetu waweze kunufaika na uchimbaji wao kuliko kutumia uchimbaji unaoitwa uchimbaji wa ramli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji wa madini unaliingizia Taifa fedha nyingi. Lakini pia uchimbaji unaendelea kwa kasi na tukumbuke kwamba tunapopata mapato tuhakikishe mazingira yetu na yenyewe tunayaweka kwenye hali nzuri. Tusiangalie ukusanyaji wa mapato tu wakati mazingira yetu yanaharibika. Wachimbaji wetu wadogo wanaharibu mazingira sana kwa kutumia miti ambayo wanaifunga kama vile matimba kuingia kwenye mashapo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nishauri ili tuweze kupunguza uharibifu wa mazingira haya basi Wizara ichukue angalau wachimbaji wachache iwapeleke nchi mbalimbali kama vile China na South Africa kwenda kuona namna gani wenzetu hawatumii miti, wanatumia utaalamu gani ama vifaa gani vya kuweza kujenga yale mashapu kutoendelea na kutumia miti, watumie utaalamu huo wa kisasa. Tutakuwa tumeokoa uharibifu wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana hili suala la uharibifu wa mazingira, sisi wachimbaji wadogo kwa kweli ni waharibifu wakubwa kwa sababu inapotokea sehemu kunaitwa lashi, watu wanachimba na zinapokata zile dhahabu wanaondoka wanaliacha lile eneo likiwa lina hali mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe kama kuna uwezekano, wakati uchimbaji huo unaendelea, waendelee kupanda miti ili iweze kusaidia kutengeneza mazingira hata ikitokea wameondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikupongeze tena kwa mara nyingine pamoja na Wizara yako. Ninamuomba Mheshimiwa Rais kama ananiona, kama kuna uwezekano basi Wizara hii atengeneze kautaratibu kazuri ka kutoa tuzo kwa viongozi hawa wenye taasisi hii kama vile Waziri, Naibu Waziri, Makatibu wake na wote kwa ujumla, taasisi hii angalau basi ipate tuzo kwa sababu tukiangalia kutoka 2017 mpaka leo 2023 mapato kupitia madini yamepanda kwa kiwango cha hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu ya Wizara Maji. Pia nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha uhai na afya njema kwa siku ya leo nakuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha nyingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya maji na hususani Wilaya ya Nyang’hwale. Tumeendelea kupokea fedha nyingi sana kwenye sekta hii ya maji hongera sana Mama tuko pamoja wana Nyang’hwale 2025 zako ni za kumwagika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa alivyofanya ziara yake Mwaka 2018 pale Wilayani kwetu Nyang’hwale na kuweza kuja kukuta mradi huu wa kichefuchefu Nyamtukuza aliweza kutoa maneno makali na maelekezo makali na mradi huo leo umeweza kukamilika. Ombi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu tunamuomba sasa aje auzindue mradi huo ambao tayari umeishakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Waziri pamoja na Naibu Waziri, pamoja na Katibu Mkuu na wizara yote kwa ujumla. Kwa kazi nzuri ambazo wamezifanya na walizozifanya katika Jimbo la Nyang’hwale kwa kweli mradi huu ulikuwa ni kichefuchefu. Alikuja Mheshimiwa Waziri Mkuu akawa anasema Nyang’hwale Oyee wanamwambia maji, akaja Waziri Aweso akasema Nyang’hwale Oyee wanamwambia maji. Lakini leo hii tatizo la maji Wilaya ya Nyang’hwale tumelipunguza kwa kiwango kikubwa sana. Hongereni sana Waziri Aweso pamoja na Prisca pamoja na timu nzima ya Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze ma–manager wangu hasa ma–manager wa RUWASA Mkoa wa Geita Jabir pamoja na Moses wa Wilaya Nyang’hwale kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya tunashirikiana nao vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja, kwanini naunga mkono hoja? Kwa kweli tulikuwa nashida ya maji katika Wilaya ya Nyang’hwale kwa kipindi kikubwa sana. Mwaka 2020 tulikuwa na asilimia 39 tu ya upatikanaji wa maji lakini kufikia mwaka 2023 tumefikia asilimia 65 kwa kiwango kikubwa tunatoa pongezi kwa wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna vijiji 40 ambavyo tayari tumeishafikiwa na maji lakini vijiji vilikuwa ni 62 bado vijiji 22. Maji yaliyopatikana ni kupitia visima virefu na vifupi lakini pia kupitia Mradi wa Maji Nyamtukuza lakini kutoka Mahando – Ilogi kwakweli maji tumeyapata hongera sana Mheshimiwa Waziri wa Maji pamoja na Naibu Waziri lakini pia pongezi nyingi zimuendee Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maji yaliyopatikana kwa kupitia Bomba la Mangu – Ilogi ni vijiji 20 mpaka sasa hivi vinanufaika na bomba hilo lakini watu wanaonufaika na maji katika Wilaya ya Nyang’hwale ni watu 133,000 kati ya watu 207,000. Mradi wa Mahando – Ilogi ifikapo 2022/2023 ampapo tunaenda kumalizia baadhi ya vijiji vitakavyokuwa vinanufaika ni vijiji vifuatavyo ikiwemo Karumwa, Busengwa, Izinya, Kayenze, Bukwimba, Mundu, Mwamakiliga, Lugwa, Kafita, Mushimba, Ikangala, Kitongo, Kakola, Nyaudele, Bungombela, Bukungu, Bulangale, Igeka pamoja na Nyamtukuza vijiji hivi vitaendelea kunufaika baada ya kukamilisha Mradi huu wa Mangwi – Ilogi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo Bajeti yetu hii ya 2023/2024 tunatarajia kukamilisha baadhi ya vijiji vifuatavyo;

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya vijiji vilivyokamilika Jimbo la Nyang’wale ama Wilaya ya Nyang’wale itakuwa imeshakamilisha na kumaliza kabisa tatizo la maji. Vijiji hivyo sitaki kuvitaja niseme kwa sababu ya muda. Tuna bilioni 15 ambazo tulitengewa kwa ajili ya mradi wa Nyamtukuza. Mpaka sasa hivi tumeshatumia bilioni 10.3, ina maana bado kuna bilioni nne na point. Mradi huo umekamilika, tunaziihitaji fedha hizo ziendelee kutolewa ili tutweze kusambaza maji kwenye vijiji ambavyo nilikuwa nataka kuvitaja.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizo ni takribani bilioni nne na kitu. Lakini pia tulitengewa bilioni nne kwa ajili ya ujenzi wa tank la chujio. Tumeahirisha kujenga chujio hilo sasa hivi tunaziomba fedha hizo ziendelee kutolewa kwa ajili ya kusambaza mabomba kwenye vijiji vingine vilivyobaki. Kwa nini tumesitisha hilo zoezi la kujenga hilo tank, ni kwa sababu sasa hivi tunatumia maji ya kutoka Mangu Kwenda Ihugi, maji safi na salama, hivyo hatuhitaji tena kujenga tank. Tunaziomba fedha hizo zitoke ili tuweze kukamilisha vijiji vyote ambavyo vimebaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache naomba kuunga mkono hoja, lakini ombi langu la mwisho, nakuomba Mheshimiwa Waziri; kwa sababu mradi huo ulikuwa ni kichefuchefu na wewe, Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wengine walifika kwa ajili ya mradi huo. Ninakuomba sasa nikuombe uje uuzindue mradi huo. Mwambie Mheshimiwa Waziri Mkuu tunawasubiri kwa hamu mje muuzindue. Lakini pia fedha hiyo niliyoiomba iendelee kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha mimi kunipa afya njema na uhai kwa siku ya leo na kuweza kusimama kwenye Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia nizidi kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambazo anaendelea kuzifanya hususani pia kwenye miundombinu ya barabara na usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kumpongeza Waziri wa Ujenzi Mheshimiwa Profesa Mbarawa pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Kasekenya, Katibu Mkuu wa Wizara pamoja na timu yote. Pia nichukue nafasi hii ya kuwapongeza wafuatao kabla ya mchango wangu; nimpongeze Meneja wa TANROADS Mkoa wa Geita, lakini pia Meneja wa TARURA Mkoa wa Geita na Meneja wangu wa Wilaya ya Nyang’hwale wa TARURA. Meneji wa TARURA Wilaya ya Nyang’hwale anafanya kazi vizuri sana kwa kushirikiana na Mameneja wa Mkoa wa Geita kwa sababu watu hawa wako karibu sana na Ofisi za Wabunge hususani Mbunge wa Mkoa wa Nyang’hwale kwa kweli wananipa ushirikiano mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuipongeza Serikali kwa kuweza kututengea bajeti kwa barabara ambayo niliuliza swali asubuhi na sasa hivi nizidi kuipongeza Serikali kwa kutenga pesa kwa ajili ya upembuzi yakinifu barabara yetu ya kutokea Nyamkumbu - Nyang’hwale – Bukwimba – Karumwa – Nyangorongo; naipongeza sana Serikali. Lakini pia Serikali imeweza kutenga bajeti kwa ajili ya upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa kilometa mbili katikati ya Mji wa Karumwa ili kuweza kupunguza vumbi na adha ya wananchi ambao wanaweza kupata madhara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua ni lini ahadi za viongozi ambao waliofanya ziara katika Jimbo la Nyang’hwale tangu mwaka 2010 wameweza kuahidi ahadi ya ujenzi wa barabara ya lami kutokea Kahama Jimbo la Msalala, Nyang’olongo – Bukwimba – Karumwa – Ijundu – Busolwa - Ngoma hadi Busisi. Viongozi hawa wakuu wa nchi wameanza kutoa ahadi hizi tangu mwaka 2010 viongozi hawa nitapenda niwataje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi hawa kwanza alianza ziara yake Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete - Rais wa Awamu ya Nne alikuja mwaka 2010 akatoa ahadi hiyo, lakini alikuja pia mwaka 2012 akatoa ahadi hiyo, lakini Mama yetu Samia Suluhu Hassan wakati anazunguka katika kuomba kura akiwa kama Makamu wa Rais na yeye aliahidi, lakini pia Rais wa Awamu ya Tano naye aliahidi ujenzi wa barabara wa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu wamekuja viongozi mbalimbali wa chama akiwemo Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi kipindi kile Abdulrahman Kinana naye aliahidi barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami.

Sasa napenda kujua ni lini utekelezaji huu wa ahadi za viongozi utaanza kwa sababu imekuwa ni hadithi leo miaka 12 nazungumzia jambo hili, viongozi hawa walituahidi sisi kama wananchi wa Nyang’hwale tunamakosa gani? Kwa sababu tumekuwa tukiahidiwa fedha zikipatikana, leo hii miaka 12 hata kwenye upembuzi yakinifu hatujaingizwa; je, ni lini tutaingizwa kwenye upembuzi yakinifu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 Mheshimiwa Rais Awamu ya Tano wakati ule alikuwa Waziri wa Ujenzi aliahidi pia, lakini siyo hivyo tu viongozi wengi wamepita na kuahidi, sasa leo mimi sitakubaliana mpaka hapo utakapokuwa umenipa majibu yaliyo sahihi, nitashika shilingi yako leo, sijawahi kushika shilingi, lakini Mheshimiwa Mbarawa leo nataka nishike shilingi ili utoe majibu yaliyo sahihi ili wananchi wangu waweze kuelewa umeahidi kitu gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukizingatia barabara hii ambayo mimi naipigia kelele miaka 12 imeunganisha mikoa mitatu, imeunganisha Shinyanga, imeunganisha Geita na imeunganisha Mwanza, lakini pia imeunganisha Wilaya tatu. Hii barabara ina umuhimu sana kwa kuchangia ama kuchochea maendeleo katika Wilaya ya Nyang’hwale. Leo hii wananchi wanaotoka ama wanaotumia barabara ya kutoka Kahama kwenda Mwanza kwa kupita njia ya Shinyanga wanatumia kilometa 280 lakini ukitoka Kahama, ukapita Jimbo la Msalala, ukapita Kalumwa Wilaya Shinyanga ukaenda Mwanza ni kilometa 160 tu kilometa zaidi ya mia moja na kitu wanakuwa wame-save. Kwa hiyo, ninaomba barabara hii muiangalie kwa umuhimu wake ili iweze kutengewa fedha kwa ajili ya kujengewa lami ili kuokoa gharama ambazo zinaweza kuepukika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ambalo inaitwa Mamang’ombe; barabara ile inaitwa Mamang’ombe ilikuwa ni barabara kuu ambayo ilikuwa ikiunganisha Kagera, Geita na Shinyanga. Barabara hii sasa hivi tuliambiwa itafunguliwa kuanzia Mbogwe itapita Bukoli, itapita Bujura, itapita Nyamigogo, itapita Nyashilanga, itapita Bumanda, itapita Kalumwa, itapita Nyungwa na kuunganisha Wilaya ya Vijijini Shinyanga, Salawi. Barabara hii tulishaambiwa na tayari kwamba ipo ndani ya mpango. Ninaomba kukuuliza Mheshimiwa Waziri mpango huo ulishafutwa au umewekwa kando kwanza? Nitapenda nijue ni lini sasa mpango huo wa kufungua barabara hiyo inaitwa Mamang’ombe ili iweze kufunguka wananchi niliowataja wa maeneo haya na vijiji vile waweze kupata maendeleo kwa sababu barabara ile imefungika. Mimi nikiwa mdogo kipindi kile kuna mabasi na malori yalikuwa yakipita kutoka Salawi kwenda Uganda kwa kupitia njia hiyo barabara hiyo imefungika tunaomba barabara hiyo iweze kufunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu ni hayo machache sitaunga mkono hoja mpaka hapo Mheshimiwa Waziri atakaponiambia barabara yangu ya kutoka Kahama - Nyangolongo - Kalumwa kwenda Busisi itaingizwa lini kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante sana. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 2) Act, 2022
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kusimama tena kwenye Bunge lako Tukufu, lakini pia niwapongeze na kuwashukuru wote ambao walioniombea dua wakati nikiwa kwenye matibabu nchini India, Wabunge wote Mwenyezi Mungu awabariki sana. Nimeweza kurejea salama na sasa hivi naendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na wachangiaji waliotangulia kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kulitumikia Taifa letu. Pia nawe nikupongeze kwa kazi nzuri ambayo unaifanya kulisimamia Bunge lako, kwa kweli tunakupongeza kazi, inakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria, nimpongeze Mheshimiwa AG kwa wasilisho lake zuri la Marekebisho Na.2 lakini pia Kifungu 432 kwa ajili ya Marekebisho ya Biashara ya Binadamu, lakini pia Kifungu Na. 95 kwa ajili ya Madawa ya Kulevya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu ni mfupi sana, kwamba nayaunga mkono marekebisho yote, lakini pia maoni ya Kamati yetu, nayaunga mkono sina pingamizi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, biashara hii ya madawa ya kulevya au biashara hii ya dawa za kulevya tumeambia tusiseme madawa ya kulevya; dawa za kulevya, tumekuwa tukipambana kuweza kuzuia biashara hii ndani ya nchi yetu pamoja na nje ya nchi kuweza kuyaingiza madawa nchini mwetu. Shughuli hii ya kupambana kuwatafuta mapapa imekuwa haina mafanikio makubwa sana kwa sababu ushirikishwaji wa wananchi umekuwa ni mdogo, mapapa haya wanafahamika, na kazi zao zinafahamika, lakini kwa bahati mbaya taarifa mbalimbali zimekuwa zikitolewa kwa ajili ya hawa mapapa lakini hazifanyiwi kazi.

Mheshimiwa Spika, napenda nitoe ushauri wangu mdogo kwa upande wa dawa za kulevya, leo hii mitaa mingi katika nchi yetu kumekuwa na mitaa maarufu kabisa ambayo inahusiana na dawa hizi za kulevya, vijana wetu wameathirika lakini Kitengo hiki cha Kupambana na Kuzuia Madawa ya Kulevya na Jeshi la Polisi limekuwa halifanikiwa kwa sababu; limekuwa halina ushirikishiaji ama ushirikishaji mzuri kupitia wananchi. Nitatoa mfano, naishi Dar es Salaam, kuna mtaa mmoja unaitwa Mtaa wa Pemba, Mtaa ule wa Pemba umekuwa maarufu sana kwa Dawa za Kulevya. Je, Kitengo hiki na Jeshi la Polisi Mtaa huo hawaufahamu?

Mheshimiwa Spika, si huko tu kuna mitaa mbalimbali iliyopo Dar es Salaam na nchi yote kwa ujumla inajulikana kwa shughuli hii ya Madawa ya Kulevya, lakini kumekuwa na usiri mkubwa sana kati ya wauzaji walio wadogo na hao wahusika Jeshi la Polisi na hawa ambao wanazua madawa ya kulevya. Kwa sababu wananchi wamekuwa wakitoa taarifa na wanakamatwa wale watu, baada ya wiki mbili au tatu, unawaona wale waliotolewa taarifa wamerudi mtaani. Hivyo, wananchi wanakata tamaa kuendelea kutoa ushirikiano, ndiyo maana hali hii inazidi kuwa mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sasa washirikishwe wananchi kwa kupewa motisha lakini wawe wanapewa taarifa, tulimkamata mtu fulani hatua zimechukuliwa na zimefikia hapa ili kuwatia moyo wananchi. Leo hii kuna ulevi mkubwa umezuka wa dawa za kulevya, mirungi, mirungi leo hii imekuwa ni kama biashara halali tunataka tujue sasa biashara hii ya mirungi imehalalishwa? Kama haikuhalalishwa kwa nini wananchi hawa ama vijana hawa ambao wamejiingiza kwenye kundi hilo wanakula hadharani na wauzaji wanajulikana na hazichukuliwi hatua. Kwa hiyo, wananchi wamerudi nyuma kutoa ushirikiano kwa ajili ya kupambana na dawa hizi za kulevya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwemo pia dawa za kulevya kama vile bangi, naomba pia nijue kwamba dawa ya kulevya bangi imehalalishwa? Dawa bangi imekuwa sasa hivi vijana wetu wadogo wadogo wamekuwa ni walevi wa hiyo kwa sababu imekuwa kama vile ni halali. Sasa tunataka tujue Serikali, Jeshi la Polisi na Kitengo hiki cha Kuzuia mmehalalisha utumiaji wa dawa hiyo ya bangi? Mtujulishe kama mmeruhusu tuweze kujua ni leseni ngapi zimetolewa kwa wauzaji hawa wa bangi. Kama ni haramu hatua gani ambayo Wizara inaichukua kuweza kuwanusuru vijana wetu, kwa sababu taarifa mbalimbali ambazo zinatolewa za wauzaji bangi na wanafahamika wanaonekana wapo mjini na wanatamba na wanaendelea na biashara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ushauri wangu naomba itolewe elimu kwa wananchi, lakini pia elimu hii itolewe kwenye shule za msingi, sekondari ili vijana wetu wakue wakijua athari kubwa ya madawa ya kulevya.

Mheshimiwa Spika, la mwisho ni kwamba, AG tunamuunga mkono, ushauri wake, mapendekezo yake na ushauri, lakini pia nalishauri Bunge liunge mkono pia mapendekezo ya Kamati ili sasa Jeshi hili ama Kitengo hiki kiongezewe meno ili kuweza kupunguza ama kumaliza tatizo kubwa la madawa ya kulevya.

Mheshimiwa Spika,ahsante sana. (Makofi)