Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Hawa Subira Mwaifunga (1 total)

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Serikali imekuwa ikitekeleza miradi ya elimu na afya nchini kwa kujenga majengo mbalimbali, lakini pamoja na Serikali kutekeleza miradi hiyo pia wananchi wamekuwa wakitumia nguvu kubwa kuhakikisha wanasaidiana na Serikali katika kuhakikisha wanajenga majengo hayo kwenye maeneo yao: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wanabainisha majengo yote ambayo ni maboma nchini ili yaweze kumaliziwa na wananchi waweze kuona thamani ya nguvu yao lakini na fedha ya Serikali inayokwenda kwenye maeneo yao ili wananchi waweze kutumia? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la ujenzi wa miradi, iwe ya elimu au afya ambayo inahusisha majengo na yasipokamilika sasa yanakuwa ni maboma, ni mkakati ambao sisi Serikali tumeuelekeza zaidi kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Tuna upatikanaji wa vyanzo vya fedha wa aina mbili; moja, kutoka Serikali Kuu. Kutoka Serikali Kuu, tunapeleka fedha kwenye halmashauri za kujenga majengo haya kwa thamani ya jengo lenyewe na kwa hiyo basi, kunatakiwa kuwa na usimamizi baada ya fedha hizi kuzipokea kuhakikisha kwamba jengo lenyewe linajengwa kwa thamani ile ile ambayo wao walitoa makadirio na Serikali Kuu kupeleka fedha kwenye Sekta ya Elimu na Afya tunapojenga vyumba vya madarasa, nyumba za walimu, matundu ya vyoo na majengo mengine, kwenye afya pia zahanati, vituo vya afya na hospitali.

Mheshimiwa Spika, pia kuna fedha ya aina ya pili inayotokana na mapato ya ndani ya halmashauri zenyewe ambapo wao halmashauri hupanga mpango wa maendeleo yao kupitia bajeti yao kwenda kujenga. Maboma mengi yanatokana na mipango ya fedha hizi za halmashauri. Kwa nini mpango wa Serikali haukukamilisha maboma?

Mheshimiwa Spika, nataka niiagize sasa TAMISEMI, kwanza iendelee na utaratibu wa kubaini maboma yote ambayo wao waliyajenga na hayakukamilika na wahakikishe wanaendelea kutenga bajeti za kukamilisha maboma hayo kwa sababu yametokana na bajeti zao. Uzoefu tulioupata wakati wa ukaguzi wa miradi hii, majengo yote yaliyopelekewa fedha za Serikali Kuu yamekwenda kama yalivyo na pale ambapo hayakukamilika hatua kali zimechukuliwa. Nao wametakiwa kukamilisha fedha kwa kuwa wameshindwa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo kwa fedha ambayo ilikuwa imepelekwa. Sasa kwa kuwa maboma mengi yanatokana na mipango yao na kushindwa kuiendeleza, bado wanatakiwa kuweka bajeti ya kukamilisha majengo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkakati wa Serikali sasa ni kuhakikisha maboma hayo yanakamilika kwa agizo hili ninalolitoa kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Kila halmashauri ifanye tathmini ya miradi yake, ione maeneo gani walianza miradi na wameshindwa kukamilisha na yamebaki maboma ambayo Waheshimiwa Wabunge sasa wanataka waone mpango wa Serikali, ili sasa wapange bajeti ya kila mwaka kuhakikisha kwamba maboma haya yanakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajua kwamba zahanati ni shilingi milioni 50, vyumba vya madarasa ni shilingi milioni 20 na fedha zote zinapatikana kwenye halmashauri. Zipo halmashauri zinapata zaidi ya shilingi bilioni tatu mpaka nne kwa mwaka, hawawezi kushindwa kupata shilingi milioni 20 ya kukamilisha chumba cha darasa, au shilingi milioni Hamsini za zahanati, au shilingi milioni 300 kwa ajili ya kujenga zahanati na kituo cha afya. Kwa hiyo, agizo langu bado linabaki pale pale kwamba tunahitaji sasa halmashauri zisimamie.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba maboma yote haya yanakamilika ili huduma zianze kutolewa kwa wananchi walioko kwenye maeneo hayo, ahsante sana. (Makofi)