Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hawa Subira Mwaifunga (25 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kuchangia katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu, mimi ni mmoja kati ya Wajumbe wa Kamati hii. Nitakayoyazungumza ndiyo ambayo tumekutana nayo na ndiyo yaliyopo. Mheshimiwa Waziri hotuba yake ni nzuri sana ukiisoma, lakini uhalisia uliomo humu haumo, kwa sababu ukienda kule uraiani, kule kwenye viwanda kuangalia uhalisia, haupo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeingia ubia na viwanda tofauti tofauti, lakini Serikali haiangalii hivi viwanda vinafanyaje majukumu yake na mwisho wa siku tunajikuta kila siku tunapoteza mapato, kila siku tutapoteza wawekezaji kwa kudhani kwamba tunaweza kufanya miujiza hii nchi iendelee kuwa ya viwanda, hakuna! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya nchi hii inatakiwa kwanza ilinde viwanda tulivyonavyo. Kabla hatujasema tunakwenda kutengeneza viwanda vingine ama kuanzisha viwanda vingine, vilindwe hivi vichache vilivyopo ambavyo vinazalisha kwa chini ya asilimia 50. Viwanda vinazalisha chini ya asilimia 50, leo tunafikiria tutengeneze viwanda vingine eti Tanzania iende kuwa nchi ya viwanda, wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vipo, lakini wafanyabiashara wenye viwanda wana matatizo mengi kweli kweli! Naishauri Serikali, Mheshimiwa Waziri, narudia tena, waendelee kukaa na wafanyabiashara wenye viwanda, wasikilizeni hoja zao, matatizo yao ili hawa basi, waliopo hapa leo waweze kuwa mabalozi wa wawekezaji wengine ambao tunawategemea waje hapa. Hatuwezi kutegemea kuleta wawekezaji wengine, wakati hawa waliopo wana matatizo lukuki ambayo yanawakabili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima kwanza tutoe haya tuliyonayo hapa, tuyarekebishe, hawa wafanyabiashara leo watakuwa mabalozi wa kwenda kututangaza vizuri nchi ya Tanzania ili iweze kuwa nchi ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa, tumekwenda kama Kamati kwenye Kiwanda cha TANALEC, tumekuta transformer zaidi ya 2000 zinatengenezwa zinakwenda Kenya. Tanzania tunaagiza transformer kutoka India, transformer 200, Mkoa wa Katavi zimelipuka baada ya kuwashwa tu! Halafu TANESCO wanawaomba TANALEC wawatengenezee zile transformer ambapo TANALEC wamegoma! Nasi tukawaambia, haiwezekani, wapeleke huko huko walikonunua transfomer hizo zitengenezwe ndiyo wazirudishe hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hili suala wanasema sijui Sheria ya Manunuzi; sidhani kama Sheria ni Msahafu! Sheria zinabadilika! Hebu Waheshimiwa Wabunge tusaidiane basi kuangalia hizi sheria wapi ni mbaya, wapi zinatatiza ili wafanyabiashara waweze kufanya biashara zao wakiwa huru, wasifungwe na hizi sheria ambazo zinawatatiza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kiwanda cha Nondo Tanzania, wanazalisha nondo nyingi kweli kweli, lakini hawana masoko! Miradi ya Serikali inakuja mikubwa mikubwa, nondo zinaagizwa kutoka nje! Tunafanya nini? Tunasema nchi ya viwanda, viwanda gani kama hivi vilivyopo havifanyiwi kazi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku kwenye viwanda watu wanaondoa wafanyakazi kwa sababu hakuna biashara! Hawa vijana waende wapi? Matokeo yake ndiyo tunakabwa kila kukicha kwa sababu vijana hawana ajira na ajira nyingi tunategemea zitoke kwenye viwanda, leo viwanda vinafungwa, hawa vijana waende wapi? Akinamama waende wapi? Hizi panya-road zitakwisha lini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, kama kweli Serikali ina dhamira ya dhati ya kutaka nchi hii iwe ni nchi ya viwanda, iende kwenye huo mfumo ambao mnasema ni wa kati, yaani watu wetu wawe na maisha ya kawaida, basi ni lazima tuboreshe viwanda nyetu vya ndani ili viwanda hivi vikifanya vizuri wawekezaji watakuja.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo nikiiangalia bajeti hii ya Serikali, TIC (Tanzania Investment Center) hawana bajeti zaidi ya mshahara. Wanafanyaje majukumu yao? Wataletaje hao wawekezaji? TBS, mamlaka nzito, kubwa inafanya kazi kubwa; ukiangalia, hawana fedha zaidi ya mshahara. Tunafanyaje mambo haya ndugu zangu? Tutafika kweli?
Mheshimiwa Naibu Spika, bado tunazungumza suala la EPZ; kwanza hii EPZ nafikiri sisi Wabunge hapa ambao tunaelewa ndiyo tunafahamu EPZ ni nini. Huko kwetu watu hawaelewi chochote. Unapowaambia habari ya EPZ, hawakuelewi! Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu ya uraia, angalau hata tunapokwenda kuomba maeneo, Watanzania wawe wanajua kitu gani ambacho kinaombewa haya maeneo ili wasiwe wagumu kutoa maeneo yao yaweze kuwekezwa hivi viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia, nenda EPZ leo, hakuna chochote kinachonunuliwa kutoka Tanzania, hakuna! Nimeuliza na nikamwuliza hata Mtendaji Mkuu pale, kwa nini hakuna chochote kinachonunuliwa hapa? Tukaambiwa tunazalisha chini ya kiwango.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, hadi vifungo ambavyo wanatengenezea mashati, suruali, wanasema tunaagiza nje! Nikauliza, tunanufaika na nini hapa kama Watanzania?
Mheshimiwa Naibu Spika, wako vijana na wanawake wamewekwa pale, ukiuliza mshahara wao, utalia! Je, hawa watu baada ya kuondoka, wanatuachia nini? Kuna teknolojia yoyote Watanzania ambayo tutabaki nayo ili kesho na kesho kutwa watoto wetu waweze kuikuta hiyo teknolojia, waweze kufaidika nayo? Hakuna! Wamejaa wenyewe pale, wako wenyewe tu. Mheshimiwa Waziri unajua, tunaomba sana Serikali ihakikishe inawasaidia Watanzania kuelewa na kufahamu kabla hatujafanya maamuzi. Maamuzi tunayafanya juu, lakini huko chini Watanzania hawana taarifa nayo! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo kuna deni kubwa! Deni la shilingi bilioni 60 limezaa shilingi bilioni 190! Mheshimiwa Waziri ukija hapa kumaliza, tuambie hizi shilingi bilioni 190.9 imekuwaje mpaka zimefikia hapa kwa mwaka mmoja, eti ni fidia! Watazitoa wapi ikiwa bajeti yenyewe ni shilingi bilioni 81? Ndugu zangu tunadanganyana hapa! Hatuna kiwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe tu Mheshimiwa Waziri, watu wa Tabora tunahitaji viwanda, tuwekee hata hicho kimoja tu kwanza, halafu mambo mengine yatafuata wakati ukiwa unaendelea na mikakati yako mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niiombe Serikali sasa, iangalie kwa umakini bajeti ya Wizara hii. Hii Wizara ni mtambuka; ni Wizara ambayo inaingiza vitu vingi sana ambavyo vipo. Hebu basi Serikali ibadilike na ione uwezekano wa kuiangalia bajeti ya Wizara hii ili kweli tuweze kufika kwenye nchi ya viwanda kama tunavyofikiria. Kama tutaendelea kusuasua, mipango ikawa mingi, mikakati mingi, fedha hakuna, haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba basi sasa ifike mahali tuamue, kama tunataka kutengeneza viwanda, tuamue tunaanza na nini? Haya mambo leo kuna hiki, kuna hiki, kuna hiki kwa bajeti ya shilingi bilioni 41 ambayo ni ya maendeleo, tunawadanganya Watanzania, hatutafika. Tunasema leo, tunaishauri Serikali leo, lakini mwisho wa siku haya maneno yataendelea kuwepo kwa sababu hakuna kinachokwenda kufanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, yangu yalikuwa hayo. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Awali ya yote ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na kuweza kusimama katika Bunge hili Tukufu ili niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze na Mkoa wa Tabora. Siku zote mcheza kwao hutunzwa. Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Tabora siku zote wamekuwa wakipiga kelele kuhusiana na suala zima la viwanda, Mheshimiwa Waziri Mwijage anafahamu, watendaji wake wote wanafahamu na wakati wote wamekuwa wakitupa ahadi za kwamba watatuletea wawekezaji katika mkoa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tabora kuna Kiwanda cha Nyuzi, kiwanda hiki alipewa mwekezaji mwenye asili ya Asia. Baada ya mwekezaji huyu kupewa kiwanda kile kitu kikubwa ambacho ameweza kukifanya katika kiwanda cha nyuzi ni kuondoa mitambo yote iliyokuwepo pale kwenye kiwanda kile kuisafirisha na kuipeleka kwao na kutuachia hall pale katika kiwanda kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hili kwa sababu nina ushahidi nalo. Ukienda katika kiwanda kile huwezi kumkuta mfanyakazi hata mmoja zaidi ya Wahindi wawili ambao wanazunguka katika kiwanda kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda kile hakinufaishi vijana wa Tabora, hakinufaishi wazawa wa Tabora na wala hakinufaishi wanawake wa Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa mwekezaji huyu aliamua kwenda mbali zaidi hadi kuamua kuuza majengo yaliyokuwa yanamilikiwa na kiwanda kile. Leo majengo yale yanatumiwa na Ofisi ya Uhamiaji pale juu, ukienda pale kwenye barabara ya Kilimatinde kuelekea kule njia ya kwenda Jimbo la Igalula utaona yale majengo. Juu wameweka ofisi ya uhamiaji chini yapo magofu tu ambayo haieleweki yanafanya kazi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Mheshimiwa Waziri atuambie ni lini basi watamwondoa mwekezaji huyu, watuletee mwekezaji mwenye nia thabiti ya kuwekeza katika Kiwanda cha Nyuzi? Malighafi za uwekezaji katika kiwanda kile zipo kwa sababu Tabora tunalima pamba, lakini pia majirani zetu wa Kahama, Shinyanga na maeneo mengine yanayolima pamba tunayopakana nayo yanaweza kufikisha malighafi zile kwa urahisi na kile kiwanda kikaendelea kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri kutuletea mwekezaji imeshindikana, kiwanda tunacho, mwekezaji waliomuweka hafai, tunaomba sana waende wakapitie kiwanda kile wakiangalie, tukifufue kiwanda cha nyuzi na sisi wananchi wa Mkoa wa Tabora tuweze kunufaika na rasilimali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tabora kuna jengo la SIDO. Kwa masikitiko makubwa sana jengo hili haijawahi kuwanufaisha hata siku moja wakazi wa Mkoa wa Tabora. Matokeo yake leo hapa ninavyozungumza, SIDO Mkoa wa Tabora wamekodisha kwa Mratibu wa Mafunzo wa VETA bwana Kaali ambaye ameweka ofisini yake pale na kutengeneza furniture na kuziuza. Hivi ndiyo yaliyokuwa malengo ya SIDO hayo ama ilikuwa ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaomba Mheshimiwa Waziri aje anipe majibu ya kunitosheleza ili niweze kujua kwa nini SIDO imepewa mwekezaji eti yeye ndiye anatengeneza makochi yake pale na furniture zake halafu Watanzania wa Mkoa wa Tabora, hawanufaiki na hiyo SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumzia ya nyumbani kwetu, sasa naomba nizungumze mambo mengine kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara wenye viwanda, wamekuwa na malalamiko mengi siku zote na kwa bahati nzuri mimi mwenyewe ni mmoja kati ya wajumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira na siku zote malalamiko haya yalipotufikia tumekuwa tukiyafikisha sehemu husika, lakini bado kumekuwa na maendeleo ya kulalamika kwa wafanyabiashara hawa kwamba mambo wanayoyahitaji kwa kweli hayatekelezwi sawasawa na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema tunakwenda kwenye nchi ya viwanda tunakwendaje kwenye nchi ya viwanda waliopo sasa yale wanayolalamikia hayafanyiwi kazi ipasavyo? Tutegemee kulete wawekezaji wengine ili waweze kufanya kitu gani kipya ambacho kitawavutia wale watu?

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iweze kuangalia hawa wafanyabiashara wetu wenye viwanda nchini. Sasa hivi wafanyabishara wenye viwanda nchini ndio wamekuwa kama vile wanatakiwa wafanye kila jambo. Kosa dogo mfanyabiashara anakwenda kutozwa faini badala mfanyabiashara huyu kupewa maelekezo nini afanye lakini imekuwa wakifika NEMC ni milioni 50, akifika Waziri ni milioni 30, sasa hawa watu watafanya kazi hii kwenye mazingira yapi? Tunawakatisha tamaa, hawa wafanyabiashara wanahitaji kuwekeza, lakini wanashindwa kutokana na mlolongo wa mambo ambayo yanawakera.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfanyabiashara yoyote au mwekezaji anapotoka nje lazima apate mwenyeji kutoka ndani ajue mwenzetu amefikia wapi, anafanya nini kuendeleza kiwanda chake, sasa mwisho wa siku itafika mahali ataanza kuambiwa mabaya kwanza halafu ndipo aambiwe yale yaliyo mema. Zaidi ya amani na utulivu ambayo ataambiwa ndilo litakuwa jambo la kwanza mengine ataambiwa hapo ukifanya hivi tayari, ukifanya hivi tayari, mambo yanakuwa si mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda kilichopo hapa Dodoma (Dodoma Wine) huyu mwekezaji anafanya kazi nzuri kweli kweli, mwekezaji huyu ana wateja wengi kweli kweli, lakini anashindwa kuzalisha kwa ufanisi kwa sababu kila kukicha akifungua ofisi yake watu wa Halmashauri hawa hapa, akifungua ofisi NEMC hawa hapa, akifungua ofisi watu wa mazingira hawa hapa. Wote hawa kila mmoja anakwenda kwa wakati wake na anahitaji fedha kutoka kwa huyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo tukumbuke huyu ameajiri, huyu anatakiwa kulipa kodi ya Serikali, huyu anatakiwa kufanya mambo kibao katika nchi hii, anafanyaje biashara zake? Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hawa wawekezaji wetu wachache tulionao ambao ni waaminifu, waweze kuangaliwa mazingira yao ya kufanyia biashara zao ili waweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha General Tyre kimekuwa ni hadithi za Alfu Lela Ulea. Niseme tu Mheshimiwa Waziri tulikwenda tumetembelea na waliahidi kwamba kiwanda hiki kingefanyiwa upembuzi yakinifu. Mwaka wa jana bajeti yake ilikuwa Sh.150,000,000 kwa ajili ya upembuzi yakinifu, leo imeandikwa Sh.70,000,000, sijui ni kwa ajili ya nini, kwa sababu ni pesa ndogo sana ambayo haiwezi kwenda kufanya huo upembuzi yakinifu ambao wanasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo majibu mengine ambayo tumepata ni sasa hivi wanatafuta mwekezaji, kwa hiyo mwekezaji mwenyewe ndio atakayekwenda kufanya huo upembuzi yakinifu. Tunasema ni hadithi za Alfu Lela Ulela kwa sababu haya mambo yameanza kusemwa tangu tukiwa wadogo tunasikia General Tyre mpaka leo bado tunaisikia General Tyre.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wenye viwanda wana malalamiko makubwa sana kuhusiana na umeme usio wa uhakika, umeme unakatikatika wakati wowote. Sasa wale wanapokuwa wameshawasha mashine zao, umeme ukikatika kwa ghafla, ukija kurudi unawasababishia hasara kubwa sana katika mitambo yao kwa sababu umeme unavyorudi haujulikani umerudi kwa nguvu ya aina gani. Kwa hiyo nimwombe Sana Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na Mheshimiwa wa Nishati waangalie kwa kiasi kikubwa ili kuona ni jinsi gani wanavyoweza kuwasaidia wafanyabiashara kwenye suala zima la umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na ziara katika Mkoa wa Tanga. Tanga ni moja kati ya mikoa inayoongoza kwa kuwa na viwanda vingi vingi sana, lakini pale Tanga umeme wa uhakika haupo. Hizo megawatt walizopewa na TANESCO haziwatoshi kuweza kuendesha shughuli za viwanda. Kwa hiyo, naomba sana wauangalie mkoa ule ili uweze kufufua vile viwanda na tayari watu wameanza kuamka kuvifufua; waweze kuleta ajira kwa Watanzania hasa vijana na wanawake ambao hawana ajira za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara wenye viwanda hasa hao wanaofanya biashara ya cement wamekuwa na malalamiko juu ya upendeleo, kwamba kuna baadhi ya wafanyabiashara wanapendelewa kwenye masuala mengine na wao hawapewi upendeleo huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanga Cement wanatengeneza clinker ambayo inatengeneza cement…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi, nimshukuru Waziri Kivuli wa Kambi rasmi ya Upinzani kwa hotuba yake nzuri. Ahsante,
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia, lakini niseme mimi pia ni Mjumbe katika Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira. Tumetoa ushauri kwenye taarifa yetu, lakini ni vema basi kuna mambo mengine ambayo tunaweza tukayazungumza angalau Wabunge wenzetu waweze kutuunga mkono katika Kamati yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningependa kuanza na suala zima la mazingira. Kwa masikitiko makubwa niseme kwamba Ofisi hii ya Makamu wa Rais siku zote imekuwa ikipewa bajeti kidogo sana pamoja na kwamba Wizara ya Mazingira ni Wizara mtambuka, lakini bado Serikali imeendelea kuipa pesa kidogo Ofisi ya Makamu wa Rais ka upande wa Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na udogo wa fedha hiyo, pamoja na udogo wa bajeti hiyo, bado fedha hii kupatikana kwake haipatikani kabisa. Tangu tulivyokutana mara ya mwisho na Ofisi ya Makamu wa Rais, mwezi Januari, kwa masikitiko makubwa mpaka leo tunavyozungumza hapa hawajawekewa hata shilingi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama tunategemea mazingira ya nchi yetu ndiyo kila kitu katika ustawi wa nchi yetu, lakini bado katika Ofisi ya Mazingira bado fedha haiendi, watumishi pale wanashindwa kutekeleza majukumu yao kutokana na uwezo mdogo wa fedha walio nao. Wameishia watu wa NEMC, sasa hivi wanachokifanya fedha ambayo wanaitumia ni fedha ya kutoza faini kwa watu. Yaani sasa hivi imefika mahali wanapata fedha kwa ajili ya makosa ya watu, sasa sijui ni Serikali ya aina gani ambayo inaendeshwa kwa fedha ambazo ni makosa ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi hali ya mazingira nchini kwetu ni mbaya sana kuliko ambavyo tunaweza kuifikiria. Tumetembea kwenye maeneo mbalimbali, lakini baadhi ya miradi ambayo ilikuwa imepangiwa kwenye bajeti hii hatukuweza kufanikiwa kuiona kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Tumetembelea eneo moja tu ambalo tulikuwa kama vile tumeenda beach, tulipelekwa eneo la ufukwe la Ocean Road; ndilo eneo ambalo pekee tulipelekwa kama Kamati kwenda kuona sehemu ambayo wanategemea kujenga ukuta kwa ajili kuzuwia mmomonyoko ambao unakuja unasogea mpaka kufikia Ikulu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maeneo mengine yote ambayo yalikuwa yamewekwa kwenye bajeti ya Serikali ya mwaka huu ya mazingira hakuna eneo lingine ambalo tumeweza kwenda zaidi ya maeneo ambayo Bunge lilitusaidia tumeweza kufika, kama Mwadui pamoja na Geita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipotembelea Mgodi wa Mwadui tulijionea hali halisi ya mazingira katika mgodi ule na kiukweli wanajitahidi kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba maeneo ya mazingira katika mgodi ule yanalindwa pamoja na maeneo ya pembezoni ambayo wananchi wanaishi. Eneo la Mgodi wa Mwadui pamoja na wananchi wake wameweza kupewa elimu ya upandaji wa miti na jinsi ya kuvuna miti ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwadui walichowafundisha watu wanaoishi maeneo ya Kishapu ni kuhakikisha kwamba hawakati miti kama vile inavyofanyika maeneo mengine. Eneo lile wamefundishwa kukata miti kwa kukata matawi na kuacha shina liendelee ili ule mti uweze kuendelea kuwa mkubwa badala ya kukata mti mzima na kuacha kisiki na kutegemea kwamba watu waendelee kupanda miti mingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelea Mgodi wa Geita. Mgodi wa Geita kiukweli kwa kuhusiana na suala zima la maji machafu wamejitahidi kwa namna moja ama nyingine kuweza kuweka bwawa ambalo linahifadhi yale maji machafu. Lakini kwenye maeneo ya mazingira, hasa kwenye maeneo ya miti kwa kweli hawafanyi vizuri kwa sababu hali ni mbaya, wananchi wanakata miti sana, wananchi wanatengeneza mikaa kwa wingi kweli kweli! Kwa hiyo, tuliwashauri angalao kwenye maeneo ambayo yanawazunguka basi waweze kusaidia wale wananchi wa pale waweze kuwa wanapanda miti na kusaidia mazingira yaweze kuwa mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikwenda kwenye Mradi wa Ziwa Victoria. Huku ni masikitiko makubwa sana, kwasababu imefika mahali hali ya mazingira katika Mradi wa Ziwa Victoria kwa kweli si nzuri na hairidhishi. Tungemuomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kwenye majumuisho yake hebu ajaribu kutuambia katika huu Mradi wa Ziwa Victoria nini hasa kinachoendelea? Kwa sababu inavyoonekana kama Tanzania tunajitahidi kwa namna moja ama nyingine kuweza kuzuia hali ya mazingira ya Ziwa Victoria kuwa sawa, lakini ukiangalia nchi jirani ambazo zinatuzunguka na tulizoingianazo mkataba bado zenyewe hazitekelezi mkataba ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tufike mahali sasa na Watanzania tuangalie na nchi jirani za wenzetu ili yale ambayo tunakubaliana kwenye mikataba yetu yaweze kufanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia kuhusu suala zima la viwanda, sasa hivi viwanda vingi vya samaki Mwanza vinafungwa na vinafungwa kwa sababu ya ukosefu wa samaki katika Ziwa Victoria. Hali ni mbaya, kiwanda ambacho kilikuwa kinaweza kufanya kazi saa 24 leo wanaweza wakafanya kazi kwa shift mbili peke yake, ikizidi sana ni shift moja. Leo viwanda vya samaki vya Mwanza baadhi vimefungwa na baadhi vinaendelea kufanya kazi kwa kusuasua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ningependa kumshukuru Waziri wa Nishati na Madini kwa kukubali mapendekezo yetu na maoni yetu ya kumuomba waanze kununua transfoma zinazotengenezwa nchini kwetu. Kiwanda cha Tanelec kinatengeneza transfoma nzuri na Mheshimiwa Waziri pamoja na Kamati tumesikia wamesema kwamba, kuanzia sasa wataanza kununua transfoma kutoka nchini kwetu. Hilo ni suala zuri naomba nikupongeze Mheshimiwa Waziri na tufanye hivyo ili kuweza kuinua uchumi wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyotangulia kusema Mjumbe mwenzangu, Wizara ya Fedha imetengewa bajeti lakini mpaka leo tunavyozungumza tunakwenda karibu robo iliyobaki kumaliza bajeti, lakini fedha iliyokwenda ni only 7 point something billion. Jamani katika bilioni 42, bilioni saba kwenye Wizara ya Viwanda ni kitu gani ndugu zangu! Nafikiri hapa tunafanya masihara, tunaweza tukawa tunalaumu, lakini mwishowa siku Serikali; Mheshimiwa Mpango na Hazina yako hebu jaribuni kuangalia basi. Zile Wizara ambazo angalao mnasema kwamba zina kipaumbele hebu zisaidieni kuziwekea fedha ili waweze kutekeleza majukumu yao badala ya kukaa mnatusaundisha (mnatushawishi) kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila wanapokuja watu wa Wizara ya Fedha ni habari ya kusaundishwa (kutushawishi) tu, lakini utekelezaji haupo. Ilifika mahali tuliwarudisha, tuliwafukuza na tukawaambia hatutakaa tusikilize taarifa yenu kwa sababu haina jipya. Kila wanapokuja wanakuja na yaleyale kumbe tatizo ni ukosefu wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hii kuna kitu kinaitwa Fair Competition, hawa watu wanafanya kazi kubwa sana, yaani hawa watu ndio ambao wanazuia bidhaa fake kuingia nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Fair Competition wanafanya kazi ngumu lakini hawana watu ambao wanafanya kazi hizo. Leo Fair Competition kati ya wafanyakazi 125 wanaohitajika wana wafanyakazi 53 tu nchi nzima. Hebu fikiria mtegemee hawa watu waweze kufanya kazi nzuri, kazi hiyo wanaifanya kutokea wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Angellah Kairuki alituelea hapa kwamba, Ofisi yake ya Utumishi imeanza kuruhusu ajira; Mheshimiwa Angellah Kairuki, sijui ajira hizo zinakwenda upande gani? Kwa sababu kama kwenye Wizara mbalimbali hakuna watumishi ambao wanaajiriwa! Mheshimwia Waziri, hebu utatueleza ukweli, hawa watumishi mnawaajiri kwenye idara zipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kusikitisha ni kwamba hawa watu wa FCC pia waafanya kazi nyingine ambazo ni za hatari sana, wanaingia bandarini wanakutana na watu, lakini…
(Hapa, kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Na mimi ningependa kuchangia katika Wizara hii na ninaomba nitoe masikitiko yangu makubwa sana kwa Wizara ya Maliasili kutokana na mambo yanayoendelea katika Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliongea na Mheshimiwa Waziri Maghembe kuhusu matatizo ambayo yamewapata wananchi wa Sikonge kutokana na Maafisa wa Idara ya Misitu na Wanyamapori walioko katika Wilaya ile. Watu hawa wanachukua ng’ombe wao, wanasukumiziwa hifadhini, wanasema kwamba, ng’ombe hawa wamefika hifadhini, wanachukua ng’ombe wanatozwa faini ya shilingi milioni mbili mpaka milioni tano kwa ng’ombe mmoja, kuna mwanakijiji mmoja ambaye ametozwa faini ya shilingi milioni 22 kwa ng’ombe wake 22 kuingia katika hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa nilimueleza Mheshimiwa Waziri nikiwa hapo na hao wananchi na aliniambia niandike, nilimuandikia, mpaka sasa ninavyozungumza Mheshimiwa Waziri hakuna suala lolote ulilolifanya. Askari hao wamefikia hatua mbaya ya kuwafanyia vibaya wananchi hawa, wanawavua nguo, wanawatandika bakora na wanawalazimisha kufanya mapenzi na miti. Mheshimiwa Waziri nilikueleza na messsage niliyokuandikia ninayo. Haya mambo hatuelewi hii nchi ni Tanzania ama hii ni nchi gani? Hawa wafugaji ni Watanzania ama hawa wafugaji ni wafugaji wanatoka nchi gani? Tunaomba sana Waziri anapokuja ku-wind up atuambie hawa wafugaji wanatakiwa waende wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kwamba nina dakika tano, naomba nimuambie Mheshimiwa Waziri, suala linaloendelea sasa hivi Kaliua, kesho kutwa wanaelekea Ulyankulu. Jambo la ajabu ni kwamba wananchi hawa walipewa hati na GN Serikali ikatangaza, matokeo yake wananchi hawa wamenyang’anywa hati zao na wanaambiwa waondoke katika maeneo ya hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa vijiji saba hawa hawaelewi kwamba watakwenda wapi, wameshakaa pale zaidi ya miaka 30 wanaambiwa waondoke, hawaelewi wataondoka waende wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niweze kumsaidia Mheshimiwa Waziri, vijiji saba hivyo ni Kijiji cha Seleli, Mwendakulima, Sasu, Kashishi, Nyasa, Iyombo na Ilega. Hawa wananchi mpaka sasa hawaelewi hatima yao, pamoja na Mkurugenzi kuwahakikishia usalama wao kwamba mpaka ripoti ya Waziri Mkuu itakapotoka ndiyo watajua kitu cha kuambiwa, lakini cha ajabu Wizara ya Maliasili inachukua hatua kabla hata hiyo ripoti ya Waziri Mkuu haijasema nini kinachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini ripoti ya Waziri Mkuu ndiyo ingekuja kutueleza kwamba, nini kifanyike, hawa watu waende wapi na ndipo wale watu wangeanza kuondolewa. Lakini leo watu wanaondolewa, wameishi zaidi ya miaka 30, wanaambiwa ni eneo la hifadhi, hawaambiwi hawa watu wanakwenda wapi? Hatuelewi huko watu wanaenda wapi, tunawatia watu hasira zisizo hata na sababu, ajabu ni kwamba Mkuu wa Wilaya ya Kaliua anasema maagizo haya amepewa na Mheshimiwa Rais, huyu Mheshimiwa Rais anayejinasibu kwa kutetea wanyonge yuko wapi aende akawatetee wanyonge wale?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mama mjamzito amejifungua ana mtoto wa siku tatu analala nje na mtoto wake, lakini cha ajabu wanatoka wanakwenda kuchoma mpaka vyakula ambavyo wale watu wamejiwekea, wanavunja nyumba wanakata mabati, wanakata miti, sasa mnawatoa watu, kama mnataka waende wakajenge kwingine haya mabati mnayakata kwa nini? Vyakula vyao mnachoma kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri aje atuambie kama ni maelekezo yeye ametoa na Wizara yake ama Mheshimiwa Rais ametoa haya maelekezo. Chonde chonde, wananchi wa Wilaya ya Kaliua wanateseka na njaa, wanalala nje bila msaada wowote na bado wanapigwa, wanawake wanabakwa na watoto hawaelewi watakwenda wapi. Haya ni mambo ya… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii. Kwanza kabisa napenda kumwomba Waziri wa Fedha na Naibu Waziri wa Fedha watupe taarifa sahihi, nzuri na itakayoturidhisha ambayo tutaweza kwenda kuwaambia wananchi wetu kuhusiana na suala zima la shilingi trilioni 1.5. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili mtaliona kama dogo mkiwa mmekaa kwenye viti vyenu lakini mkienda kule kwa wale ambao mnadhani hawajui masuala ya uchumi ni zito na ni kubwa na wanahitaji majibu ya kuridhisha. Mheshimiwa Naibu Waziri alitujibu hapa hata sisi Wabunge wengine ambao hatujui masuala ya kiuchumi tunajiita mabushi uchumi hatukumuelewa alichotuambia. Watakapokuja kumalizia tunaomba watuambie na watupe kauli ya Serikali wapi iko shilingi trilioni 1.5? Ili na mimi nikitoka hapa nikienda kumwambia mwananchi wangu wa Itonjanda kule Tabora aelewe hii shilingi trilioni 1.5 imetumika vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye bajeti. Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hatua yake ya kuamua kwenda kwenye Kiwanda cha Urafiki. Sisi kama wajumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira tulikwenda pale na yale aliyokutana nayo Mheshimiwa Waziri Mkuu ni masuala ambayo na sisi kama wana Kamati tulishauri na tuliiomba Serikali iende pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda kile Serikali ya Tanzania inakimiliki kwa asilimia 49 na China inamiliki kwa asilimia 51. Kwa yanayoendelea pale, tungeiomba sana Serikali na kwa sababu na Waziri Mkuu amekwenda ni afadhali tukamiliki sisi wenyewe ili tuweze kupata faida inayotokana uzalishaji ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, demand ya nguo za Kiwanda cha Urafiki ni kubwa sana nchi kwetu kuliko hata ambavyo watu wanafikiria. Siku tulipokwenda pale tulikuta msururu wa magari umepaki pale unasubiri mzigo utoke kiwandani ili waweze kusafirisha. Cha ajabu mzigo hakuna kwa siku wanatengeza khanga chache na nafikiri ndani ya miezi sita ama saba iliyopita walishafunga kabisa hata huo uzalishaji. Hayo ambayo Waziri Mkuu alitaka kuyajua hata sisi Kamati tuliuliza mashine zetu mmepeleka wapi? Hizi mlizoleta mbona hamjazifunga mnasema ni mbovu, leteni zile za kwetu kwanza halafu na hizi mlizonunua ambazo ni mbovu zirudisheni mtuletee nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wizi wa hali ya juu katika nchi hii. Wakati Waziri wa Viwanda akisisitiza viwanda aanze na Kiwanda cha Urafiki ambacho tunamiliki asilimia kubwa sana, asilimia 49 siyo mchezo, hiyo asilimia moja kuichukua ni rahisi sana tukisema jamani sasa ninyi basi mmeshindwa kuzalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna viwanda vya khanga Morogoro vya Textile, viwanda vya khanga vya Nida, vinafanya kazi vizuri sana na ukienda sokoni khanga za Nida na Morogoro ni nyingi ziko wapi khanga za Kiwanda cha Urafiki? Kwa nini Nida na Morogoro wanaweza Urafiki wanashindwa? Lipo tatizo na tatizo hili tunaomba liangaliwe. Tunamshukuru Waziri Mkuu ameingilia kati tunaamini kabisa sasa hivi Urafiki itaanza kufanya kazi kwa faida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee kuhusu Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe. Hili neno la Liganga na Mchuchuma nimekuwa nikilisikia toka nikiwa binti mdogo sana. Kwanza nilikuwa naona kama ni kitu fulani cha kuchekesha, nilikuwa sielewi lakini nimeelewa hii Liganga na Mchuchuma ni kitu gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la makaa haya ya mawe linakadiriwa kuwa na zaidi ya tani milioni 428 na wanasema tunaweza kutumia kwa takribani miaka 500 kwa mujibu wa NDC. Chuma kiko zaidi ya tani milioni 126. Hivi ndugu zangu utajiri huu wote tulionao toka tumeanza kusikia Liganga na Mchuchuma, hatujawahi kusikia tumepata mafanikio gani kwenye hili. Hivi hizi pesa ambazo tunazitoa kutakwenda kununua Bombardier, kujenga viwanja vya ndege, kujenga kuta Mererani kwa nini tusiwekeze kwenye mradi huu ambapo tutapata faida kubwa na ya haraka kabisa. Ndugu zangu tutakapochimba wenyewe chuma chetu tutapata faida kubwa kwelikweli katika hii nchi ya Tanzania ya viwanda ambayo tunaizungumzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na kauli mbiu ya Tanzania ya Viwanda na imekuwa ikizungumzwa sana. Mpaka tunakwenda kumaliza bajeti hii, Wizara hii imepata asilimia 9 peke yake ya fedha za maendeleo. Halafu tunasema hii ni Tanzania ya Viwanda, ndugu zangu Tanzania ya Viwanda ipi? Asilimia 9 peke yake kwenye fedha za maendeleo halafu tunajinasibu kwamba Tanzania ya Viwanda, kwenye viwanda vipi? Watendaji wa Wizara ukiangalia maelezo yao na taarifa zao wana mikakati mizuri kwelikweli ya kuijenga Tanzania ya Viwanda lakini hawana pesa. Kwa nini tusiwasaidie ili waweze kutimiza azma ya Mheshimiwa Rais ya Serikali ya Viwanda? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kumekuwa na fungua fungua ya viwanda vingi sana, tunaambiwa tuna viwanda 3,306, mimi sijawahi kuviona na Mheshimiwa Mwijage anajua hatujawahi kuviona lakini takwimu ndiyo zinavyosema na zinavyoonyesha. Viwanda hivi pamoja na kufunguliwa lakini vipo vingine ambavyo vinafungwa kutokana na ukiritimba wa mambo mengi ikiwepo mambo ya kodi za hovyo hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwa kwenye Kamati lilikuja suala la sukari ya viwandani. Naomba hili niwaambie Wizara ya Fedha, mambo haya mnayafanya mwisho wa siku ng’anya linakuja kuwashukia Wizara ya Viwanda. Ninyi ndiyo mnatakiwa mtoe vibali na msababishe sukari ile iweze kutolewa mwisho wa siku hamtoi na kusababisha viwanda kufungwa. Kiwanda cha Sayona kilifungwa kwa sababu kilikosa sukari. Matokeo yake unaambiwa Wizara ya Viwanda haifanyi kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliletewa list ya viwanda 10 ambavyo walisema tayari vimeshapata vibali vya kutolewa sukari, lakini mpaka tunamaliza kikao cha Kamati walikuwa hawajapata. Nami naendelea kushauri Serikali, kama hawa wafanya biashara wanashindwa kulipia kodi za pale bandarini tengenezeni bonded warehouse muweke hizo sukari ili hawa wafanyabiashara wakishakuwa tayari waweze kuchukua mzigo wao wafanye biashara. Leo mmezuia, mnawadai madeni makubwa ambayo na wao wanashindwa kufanya uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine kuna sababu gani ya sukari hii isitozwe kodi ili kupunguza huu urasimu ambao mnausema, mnauona, mnaudai na mnaujua. Kwa nini msitoze kodi? Kwa nini msifanye kama sukari ya kawaida inayoingia ili mfanyabiashara ajue nikiagiza sukari ya kiwandani nitalipa kodi kuliko ilivyo hivi sasa hawalipi kodi lakini mwisho wa siku kumekuwa na urasimu wa hali ya juu. Hali ni mbaya, baadhi ya wafanyabiashara ambao wanaotengeneza bidhaa zinazotumia sukari wanahangaika, wanateseka kupata hiyo sukari waambieni kama kuna kodi waweze kulipa ili maisha yao yaweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu suala la biashara. Watu wanafunga biashara kwa sababu kuna mambo yanayowakera. Mimi kama mfanyabiashara niambieni natakiwa kulipa kodi kwa mwaka kiasi gani nilipe, nikishamaliza hapo niacheni nifanye biashara yangu. Leo kumekuwa kuna ufuatwaji wa wafanyabiashara mpaka inaleta kero. Kuna baadhi ya wafanyakazi wa TRA wasiokuwa waaminifu, mmewatengenezea mazingira ya rushwa ya ajabu, Mheshimiwa Dkt. Mpango nilimwamba hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wafanyabiashara na wafanyakazi wa TRA wamekuwa wanachukua watu wanakwenda kwenye maduka, ananunua kitu cha Sh.20,000 au Sh.50,000, nimeshuhudia mwenyewe kwa jicho langu, anaambiwa subiri risiti anasema nina haraka. Dakika tano nyingi anarudi na watu wa TRA wanakwenda kumdai mtu Sh.3,000,000 kwamba hujatoa risiti, nimelishuhudia mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanapoomba hizo Sh.3,000,000 wakiona mfanyabiashara hataweza kulipa hela hiyo wanaomba rushwa. Kauli wanazotumia wanasema utatoa mita, ukiambiwa kutoa mita ni Sh.1,000,000, ukiambiwa kutoa nusu mita ni Sh.500,000. Mimi ni mwakilishi wa wananchi niliuliza hilo suala na Mheshimiwa Dkt. Mpango TRA wapo wengi, hawa vijana mnaowatuma kwenda kufanya hiyo shughuli huko wanakera sana wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sehemu iliyokuwa na tatizo la kupata mlango wa biashara kama Kariakoo. Leo milango Kariakoo inatangazwa. Ukifika unaambiwa mlango huu unakodishwa watu wamefunga biashara zao.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naomba nami nichangie haraka. Nilikuwa napitia jedwali la TAMISEMI katika pesa za ujenzi wa hospitali za Wilaya nimeshangaa sana kuona Manispaa ya Tabora haijawekewa hata shilingi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utakumbuka Mheshimiwa Waziri Madiwani kutoka Manispaa ya Tabora tulikuja ofisini kwake, moja kati ya maombi ambayo tulimwomba ni kuweza kutusaidia Hospitali ya Wilaya ijengwe. Nafahamu kwa nini amefanya hivi, akiamini kwamba Hospitali ya Kitete itaweza kutusaidia watu wa Manispaa ya Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Kitete ina matatizo mengi, hospitali ya Kitete ina changamoto nyingi. Kwanza haina Madaktari, mpaka sasa kati ya Madaktari tisa bingwa wanaotakiwa kuna Daktari mmoja peke yake. Ukimuuliza Daktari huyu ubingwa wake amesomea kwenye nini wala haelewi, lakini ni Daktari Bingwa peke yake ndiye aliyepo katika hospitali ya Kitete. Leo hospitali ya Kitete ni hospitali ya Rufaa, kwa hiyo wale wananchi wote wa Manispaa ya Tabora wanapokuwa wana matatizo wanakimbilia hospitali ya Kitete, imekuwa na msongamano mkubwa kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha ajabu pale kuna majengo ya chuo ambayo sasa yameanza kuchakaa, hebu atueleze atakapokuja ku-wind up ni lini yale majengo yatamaliziwa na watafungua kile chuo ili tuweze kuondokana na upungufu wa Madaktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hiyo ya Kitete ina jengo la ICU lakini hakuna mashine hata moja katika jengo hilo na ndiyo hospitali ya Rufaa, leo bado mnatuona kwamba watu wa Tabora hatuhitaji kupewa hospitali ya Wilaya tuendelee kutumia hospitali ambayo ina matatizo chungu nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Kitete wodi ya wazazi ni ndogo sana, kwa siku katika Hospitali ya Kitete inapokea akinamama 15 mpaka 17 wanaotaka kujifungua kwa kawaida, inapokea akinamama watano mpaka saba wanaokwenda kujifungua kwa operesheni, wodi ile haitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo nafasi kubwa kwenye ile hospitali, tunaomba kwa sababu ni hospitali ya Rufaa lijengwe jengo kama lililopo Hospitali ya Mwananyamala ama lililopo pale Sinza ili liweze kusaidia akinamama hawa kuondokana na matatizo ya kuwa na msongamano wa hali ya juu. Wanawake pale wanalala chini, wanawake pale wanaenda kujifungua wanalala wawili na watoto wao, kwa kweli haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungeomba badala ya kutubana, kutegemea hospitali ya Rufaa ambayo ina msongamano mkubwa, tunaomba nasi basi tutengewe fedha ili tuweze kujenga hospitali yetu ya Wilaya. Tunashukuru kwa pesa katika Wilaya ya Uyui na Wilaya ya Sikonge, tunaomba na Tabora Manispaa itengewe fedha ili tupate hospitali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji pia standby jenereta; katika Hospitali ya Rufaa ya Kitete hakuna jenereta, hata kama mtu anafanyiwa upasuaji kama umeme unakatika na umeme wenyewe huu, haiwezekani na watu wanaweza wakafia na wengi wanakufa wakiwa wanafanyiwa operation kwa sababu umeme unakatika mara kwa mara. Tunaomba wamtusaidie hospitali ile angalau basi iwekewe standby generator ili kuokoa maisha ya Watanzania walio wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la elimu. Shule za zamani tunashukuru tumepiga kelele angalau zimefanyiwa matengenezo. Shule ya Tabora Girls, Shule ya Tabora Boys na Shule ya Mirambo, tunawashukuru sana kwa hilo lakini bado zipo changamoto. Ningeomba sana Mheshimiwa Waziri Tabora Girls wasichana wanalala chini kwa sababu vitanda vingi pale vimevunjika, wanaomba wasaidiwe angalau vile vitanda viweze kutengenezwa waweze kulala kwa nafasi. Pia Tabora Girls ina uhaba wa Walimu. Kwa hiyo, tunaomba watusaidie Ofisi ya Utumishi waajiri Walimu, wale waliowandoa wasiokuwa na vyeti waturudishi Walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaomba na bado tutaendelea kuomba kama wanawake angalau kwenye shule kama hizi, basi wanawake wale mabinti waweze kusaidiwa taulo, kwa sababu waliopo katika shule hizi wengi ni wale ambao wazazi wao hawana uwezo, kwa wale ambao wazazi wao hawana uwezo waweze kusaidiwa taulo ili angalau wanapofika kwenye kipindi chao cha hedhi waweze kuwa salama na waweze kuendelea na masomo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Ofisi ya Makamu wa Rais na nitajikita zaidi kwenye suala zima la mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe masikitiko yangu makubwa sana kuhusiana na bajeti ya Wizara hii. Kama ambavyo hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani imesema imekuwa ni mazoea kwa Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira kutokutengewa bajeti ya kutosha na hata hiyo kidogo ambayo inawekwa haifiki kama ilivyokusudiwa, hivyo kupelekea ufanyaji kazi katika hii kuwa mgumu kuliko ambavyo tunatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo tunafahamu suala zima la mazingira ndiyo roho za sisi Watanzania. Tunapodharau mazingira tutegemee tutapata elimu na afya tunajidanganya. Bila mazingira hakuna afya, elimu na miundombinu vinginevyo tunajisumbua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisikia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wakizungumzia kuhusiana na sula zima la ukatazaji wa matumizi ya mifuko ya plastiki. Bahati nzuri niko kwenye Kamati ya Mazingira, suala hili lilianza muda mrefu na sisi kama Kamati tulijaribu sana kuishauri Serikali na kuangalia ni kwa namna gani wanaweza wakafanya ili kusaidia hawa wenye viwanda ambao wanatengeneza mifuko ya plastiki waweze kutengeneza kwa teknolojia ya kisasa. Teknolojia za kisasa zipo ambapo mifuko hii mingine watu wanatengeneza na inaoza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama Serikali imejiandaaje baada kuzuia matumizi haya kwa nchi jirani ambazo zinazalisha kwa wingi kuliko tunavyozalisha Tanzania mifuko ya plastiki kuingia nchini kwetu? Kwa sababu ni ukweli usiopingika Tanzania tunazalisha mifuko ya plastiki kwa asilimia 30 peke yake lakini asilimia 70 ya mifuko ya plastiki inayoingia nchini kwetu ni mifuko inayotoka nje ya nchi. Je, Serikali imejipanga namna gani kuhakikisha kwamba mifuko hii haiwezi kuingia nchini Tanzania na matumizi ya mifuko ya plastiki yakaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati tunakataza mifuko ya plastiki tumejiandaa na vifungashio vya aina gani? Kwa sababu nachokiona hapa ni makatazo tu lakini hatujaambiwa kwamba tunakwenda kutumia mifuko ya aina gani, leo tutakuwa tunabeba mikononi bidhaa ama tutakuwa tunafanyaje? Kwa hiyo, tungeomba sana Waziri anapokuja hapa atuambie ili Watanzania wajue baada ya mifuko ya plastiki kukatazwa tarehe 1 sijui Mei au Julai, nini ambacho kitatumika mbadala badala ya mifuko hii ya plastiki? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ya mazingira ni mtambuka kama nilivyosema, kwa hiyo lisiishie kwenye masuala ya mifuko ya plastiki peke yake, je, suala la mkaa limefikia wapi mpaka sasa? Kwa sababu ya kupata mkaa watu wanakata sana miti. Leo tunaambiwa nchi inakwenda kuwa jangwa kwa asilimia 61, hii ni asilimia kubwa sana kwa nchi ya Tanzania, tunapoelekea vizazi vyetu vitakuja kukuta nchi imeshakuwa jangwa, hali ni mbaya kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapofikiria zaidi mifuko ya plastiki, mimi huwa nasema vitu vidogo vidogo Mheshimiwa Waziri anajua, tusing’ang’anie na vitu vidogo vidogo kama mifuko ya plastiki tuangalie uhalisia wa mazingira, vitu vingi zaidi vinategemea mazingira yetu. Kama mazingira hayataboreshwa tusije tukategemea hivi vyote ambavyo tunavifanya vitaendelea kuwepo kwa sababu ni lazima vitapotea kutokana na kwamba mazingira siyo rafiki, tunakwenda kuingia kwenye ukame wa hali ya juu. Kama ambavyo mmeshuhudia kuna maeneo ambayo mvua hazijanyesha kabisa, kuna maeneo kama kwenye Mikoa yetu ya Tabora tulikuwa tunapata mvua misimu miwili, leo Tabora ukienda ni msimu mmoja tu ndiyo mnapata mvua na mvua zenyewe siyo za zinatosheleza, hali ni mbaya kweli kweli kila maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Serikali iangalie upya kuhakikisha kwamba bajeti inayotakiwa katika Ofisi ya Makamu wa Rais inapelekwa kama ilivyokusudiwa kuliko kutegemea bajeti za wafadhili. Hawa wafadhili leo umeomba bajeti ya asilimia 40 unaletewa bajeti asilimia 10, mwisho wa siku mambo yanakuwa hayaendi ama hawaleti kabisa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kusimama hapa katika Bunge hili Tukufu na kuchangia hoja ya Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa sana nieleze kuhusu bajeti katika Wizara hii, kwa miaka mitatu mfululizo sasa bajeti ya Wizara ya Viwanda imeendelea kushuka siku hadi siku. Mwaka 2016/2017 bajeti ilikuwa ni asilimia 42.37; mwaka 2017/2018 ilikuwa asilimia 30.64; mwaka 2018/2019 ilikuwa ni asilimia 24.28, hiyo ni fedha ambayo inapelekwa katika Wizara ya Viwanda na Biashara. Kauli mbiu ya CCM ya Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Magufuli ni uchumi wa kati, Tanzania ya viwanda. Tanzania hii ya Viwanda inafikiwaje kwa bajeti ya aina hii? Hivi kweli tuko serious kabisa kwamba tunahitaji uchumi wa kati kwa Watanzania kama hata bajeti ya Wizara inayohusika na masuala ya viwanda na biashara bajeti inakwenda kwa kiwango hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara na siku zote nimekuwa nikijiuliza hivi wenzangu Wabunge wa CCM ambao tuko nao kwenye Kamati, hivi mko serious kweli kabisa kwamba hii kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais mnaishikilia kidedea? Maana kila Mbunge wa CCM akisimama hapa ni Stiegler’s Gorge, ni standard gauge ni ndege sijui hiyo haikuwa kauli ya Mheshimiwa Rais wakati anaomba kura. Haya yamejitokeza kila siku wanayasifia haya, hebu watuambie, hii Tanzania ya viwanda iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu anayeonekana kinara wa Tanzania ya Viwanda ni Mheshimiwa Rais peke yake. Kila anapokwenda atasimamia suala la viwanda lakini hakuna anayemsaidia kwenye suala hili. Amezungumza Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani, hivi kweli Waheshimiwa Mawaziri waliopewa dhamana kwenye hii Wizara wanadhani wanaitendea haki. Hawaoni kwamba wanaenda tofauti na kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais na kwenda tofauti na kaulimbiu ya Rais ni kukiuka maneno ya Mheshimiwa Rais. Hebu niwaombe sana tuwe serious kwenye hili, Wizara ya Fedha pamoja na fedha kuwa kidogo lakini hebu waangalie vipaumbele tumezidi kuwa na vipaumbele vingi, inafika mahali hata kile kipaumbele ambacho walikikusudia hakitekelezeki. Halafu tunaimba Tanzania ya Viwanda, Mheshimiwa Rais akienda kuzindua viwanda anafurahi, lakini unashangaa anafurahi leo, kesho TRA wanakwenda pale kila kiwanda kinakwenda kufungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa sana tumeshindwa hata kuvilinda viwanda tulivyonavyo nchini. Leo viwanda vilivyopo nchini vinazalisha kwa ubora wa hali ya juu, lakini utashangaa hata Serikali yenyewe inapotengeneza miradi inakwenda kuagiza nje. Sasa hawa wanaotengeneza humu ndani nani atanunua bidhaa zao. Tunaagiza bidhaa nyingi kutoka nje, tunawapa zero rate, matokeo yake bidhaa zile zinazotoka nje zinakuwa bei ndogo kuliko bidhaa za ndani na humu ndani watu wanawachaji kodi, kuna umeme, kuna wafanyakazi, kuna regulatory authorities chungu nzima ambazo zote hizo wafanyabiashara hawa wanatoa fedha. Wanajikuta wanashindwa kufanya uzalishaji wa kutosha kwa sababu ya gharama za uzalishaji na leo bado sisi kama nchi tunaendelea kuendekeza kuingiza vitu ambavyo hata Tanzania tunazalisha tena kwa kiwango cha hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba nitoe wito kwa Serikali kama kweli tunataka Tanzania iendelee kuwa ya viwanda hivi viwanda tulivyonavyo hebu tuvilinde tuwalinde hawa wafanyabiashara wenye viwanda waliopo nchini kwa sasa, wenye moyo ambao bado hawajakimbia. Kama hali ikiendelea namna hii, kama kiwanda kilikuwa kinazalisha kwa asilimia 80, leo kiwanda kinazalisha kwa asilimia 15, kuna tija namna hiyo jamani, halafu tunasema hii ni Serikali ya viwanda, Serikali ya viwanda ipi jamani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza wenzangu lakini nami naomba nikazie, TRA ni mwiba mchungu sana kwa wafanyabiashara. Wafanyabiashara wamelalamikia sana TRA, sio rafiki tena wa mlipakodi, badala yake amekuwa ni adui mkubwa sana wa mlipakodi, badala ya TRA na mlipakodi kuwa marafiki, kukaa, kuzungumza na kuona ni kwa namna gani ambavyo wanaweza wakalipa kodi, TRA wamekuwa wababe, TRA hawataki kusikiliza, TRA inatukosesha mapato, TRA inasababisha maduka yanafungwa, TRA inasababisha viwanda vinafungwa. Leo nilikuwa namsikia mtu wa TRA anasema biashara zaidi ya milioni moja zimefungwa, huo ndio ukweli, kama kuna watu wamesikiliza clouds asubuhi, zimefungwa ndio!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tuone sasa, tunachokiangalia tuna- target kitu gani, tunataka kodi, lakini kama tunataka kodi na maduka yanafungwa kodi hizo tunazipata wapi? Tunataka kodi, viwanda vinafungwa kodi hizo tunazipata wapi? Leo viwanda vinapofungwa, ajira pia zinapungua, kwa hiyo tuone ni kwa namna gani tunavyoweza kuweka mfumo mzuri ama kuiangalia TRA kwa jicho la tatu, inawezekana wako watu ambao wana mpango wa kukwamisha hii nchi isiende mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nieleze kwa masikitiko makubwa sana kuhusiana na suala zima la viwanda vilivyobinafsishwa ambavyo vingi havifanyi kazi. Mara zote tumekuwa tukiipigia Serikali kelele mtueleze mna mpango gani na hivi viwanda vilivyobinafsishwa? Ukiuliza kwa watendaji wao wanafuata sheria na utaratibu lakini niwaambie Watanzania mikataba iliyoingia kuwauzia viwanda watu hawa ni mibovu ambayo inasababisha hivi viwanda sisi kama Watanzania tutashindwa tena kuvifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikumbuke kauli ya Mheshimiwa Rais amesema hawa watu ni wahujumu uchumi. Leo mtu amenunua kiwanda kazi anayofanya anapanda maua. Tumekwenda kwenye kiwanda kimoja Arusha, kiwanda kinazalisha vizuri sana, kinalipa kodi vizuri sana lakini eneo walilonalo ni dogo. Kwa muda mrefu sasa wanaiomba Serikali eneo la nyuma ya kiwanda chao ambapo kuna kiwanda kingine kinatumika kupanda maua ili waweze kuongeza uzalishaji kwenye kiwanda chao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili limeshindikana na tunamuuliza Waziri tatizo ni nini na wao nafikiri bado hawajajua tatizo kwa sababu Naibu Waziri hakuwa na majibu ya kutuambia. Hata tulipokuja kwenye kikao tunamuuliza Naibu Waziri wamefikia wapi kuhusiana na suala hilo hakuwa na majibu ya kutuambia. Leo katika Bunge hili tunaomba mtuambie Serikali mna mpango gani wa kuwapa TBL eneo hilo wanaloomba ili waongeze uzalishaji ili muendelee kupata kodi badala ya ilivyo hivi sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tangu suala la viwanda lipelekwe kwa TR, hili Waziri wa Fedha atuambie ni lini Waziri wa Fedha mtatusaidia kuturejeshea viwanda vyetu kwa sababu viwanda vyote viko chini ya TR? Kama viko chini ya TR, Wizara ya Viwanda haina mamlaka na viwanda hivi, kwa hiyo, kila tunavyowauliza majibu yao ni kwamba wao hawana mamlaka ya viwanda hivi. Ningeomba wakati wana windup Wizara ya Fedha ituambie viwanda vilivyobinafsishwa lini vitarudishwa Serikalini ili watu wanaovihitaji waweze kuvifanyia kazi?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Hawa Mwaifunga.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu katika Bunge hili la Bajeti.

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Mheshimiwa Freeman Aikaeli Mbowe, kwa kuniteua katika kipindi hiki kifupi kuwa Naibu Waziri Kivuli kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Namshukuru sana kwa kuniamini na namwahidi sitamwangusha na sitawaangusha wenzangu. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Hawa inaelekea safari hii wamepewa wanawake watupu. Inakuwaje hii?

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Yah! Inaonesha kwamba ni kwa namna gani wanawake tunaweza kufanya kazi vizuri na kwa uaminifu mkubwa na tukipewa majukumu tunaweza kuyatekeleza kwa uaminifu. (Makofi)

SPIKA: Kwamba Mheshimiwa Mbowe ana imani sana na akina mama, ahsante sana. Endelea tu. (Makofi/Kicheko)

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, naanza kuzungumzia kwa upande wa suala zima la afya na kipekee kabisa nizungumzie suala la Corona, suala linaloendelea katika nchi yetu kwa sasa. Corona imefika, ipo Tanzania, nami naomba sana pamoja na wenzangu wengi kulielezea vizuri sana suala hili la Corona. Napenda sana niwakumbushe akina mama wenzangu, akina baba kuona ni namna gani tunafuata maelekezo ya wataalam wetu wa afya. Tusidharau jambo hili kwani lipo, tutakufa tutaacha watoto wetu; watoto wetu watakufa watatuacha wazazi, inaumiza sana. Tunaoa kwa wenzetu, kwa hiyo, tunaomba sana tujitahidi kufuata maelekezo ya wataalam wetu wa afya.

Mheshimiwa Spika, watu wengine wameshauri kwamba kuwe na angalau mambo mbadala ambayo yanaweza yakafanyika. Hata hivyo kuna mambo ambayo yanaendelea kwenye mitandao ya kijamiii ambayo ni mbadala yanatisha. Yaani unakuta mtu anakwambia chemsha sijui miarobaini, weka tanganwizi, weka ndimu, ukichemsha mpaka unaona yale mapovu yanatoka, mtu anatia kwenye kikombe anakunywa. Jamani, tutauana.

Mheshimiwa Spika, ningeomba sana kwa sababu Mheshimiwa Dkt. Ndugulile unafahamu kabisa pele Muhimbili kuna chuo maalum cha tiba asilia tusaidieni ndugu zangu tutakufa. Kuna mtu juzi alikuwa ana-blend kabisa zile Ndimu anachukua anaweka kwenye Blender ana-blend ameweka pamoja na Tangawizi mule ndani katia kwenye glass na akatoa tahadhari kwamba jamani hii dawa ni chungu kweli kweli lakini Mtu akisikia kwamba inasaidia anafanya anachoweza kukifanya. Tunaomba sana mtusaidie hili janga linatisha na kila mtu anaogopa tunahitaji kupona ndugu zangu na tuendelee kumuomba Mwenyezi Mungu tumuweke kwenye maombi kila mtu kwa dini yale ili janga hili liweze kutuepuka lisije likafika kama walivyofikiwa wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna namba ambayo imetolewa katika kipeperushi cha Mheshimiwa Waziri wa Afya. Namba ile unaweza ukapiga leo ikapokelewa kesho, hii ni hatari sana. Hizi namba watu wanapopiga hii namba ambayo imetolewa kwenye kile kipeperushi ni muhimu sana pengine wana taarifa sahihi kuhusiana na suala la watu ambao wako kwenye maeneo yetu tayari wana maambukizi, tayari wanaonesha dalili lakini hawataki kujitokeza. Kwa hiyo, tunaomba sana kama hii namba inakuwa haiwezekani kupokelewa ziwekwe hata tatu, nne, tano ili angalau kuwe na watu wanaoweza kupokea na kuweza kusaidia nduguzanguni lakini vinginevyo hii namba moja haipokelewi na malalamiko yamekuwa mengi. Kwa hiyo, ningeomba sana Wizara iangalie jambo hili, Serikali iangalie jambo hili, jambo hili ni muhimu, jambo hili ni nyeti, tutakwenda kupona kama tutaambizana ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hotuba ya Waziri Mkuu kuzungumzia masuala mazima ya afya lakini kuna changamoto nyingi sana katika sekta hii ya afya; kwanza bajeti inayotoka huwa ni ndogo pamoja na changamoto zilizopo lakini pili; tumekuwa tukiambiwa zaidi kwamba bajeti inaongezwa kwenye dawa, kwenye dawa, kwenye dawa lakini mgonjwa utampa vipi dawa kama hajapimwa na kugundulika ugonjwa wake? Kwa hiyo, nilidhani hasa kwenye hospitali zetu za rufaa tujitahidi sana Serikali kupeleka vifaa vya kupimia kwa sababu unakwenda wkenye hospitali, unafika kwenye hospitali ya rufaa.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano; nikitolea mfano hospitali ya Kitete-Tabora, unafika pale kuna mgonjwa ana matatizo ya moyo unambiwa machine ya ECO imeharibika ukimuuliza tangu lini imeharibika? Ina mwaka haifanyikazi, mashine ya ECG imeharibika ukimuuliza imeharibika tangu muda gani mpaka leo kabla sijaja humu ndani ya Bunge nimempoigia simu Daktari na kumuuliza mashine imepona ama haijapona? Kaniambia imepona sasa kama imepona kweli ama alikuwa ananidanganya lakini ukweli ni kwamba mashine ilikuwa ni mbovu. Mtu anapewa rufaa kutoka Urambo, kutoka Kaliua, kutoka Ulyankulu aende Kitete, akifika Kitete nako hapati ile huduma anapewa tena rufaa ya kwenda hospitali ya Bugando sasa kuna maana gani ya hospitali kuiita ya rufaa kama haina hata vifaa vya upimaji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hayo hayo nimeyaona katika hospitali ya Mwananyamala. Nimefika pale nimekwenda kutibiwa nimekuta wazee wengi sana wamekaa pale wakienda kupima moyo. Roho iliniuma sana nimefika pale ilibidi niondoke kabla sijafanya chochote kwa sababu wangeona mimi natangulizwa kuanza kuingia mule ndani wangeumia sana nikajisikia vibaya. Imefika muda wangu kuingia nafika kuna mashine tatu zote zimeandikwa tarehe mpaka na mwaka mashine zile zilipoharibika. Mashine imeharibika tarehe 09.05.2016 ya ECG machine, ya ECO mpaka leo mashine ile haijatengenezwa. Kipo kimashine kidogo tu ambacho ndiyo kinatumika kwa msururu ule na ile ni hospitali ya Mkoa sasa kwa kweli hali ni mbaya. Tungeomba sana pamoja na bajeti mnazoziongeza kwenye dawa ongezeni basi na bajeti kwenye vifaa vya kupimia kwa sababu hizi hospitali zetu za rufaa watu ndiyo tunazozitegemea. Hali ni mbaya kuliko ambavyo tunaelezwa, kwa hiyo niseme tu pamoja na dawa lakini na vifaa hivi viongezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la utoaji wa dawa pia limekuwa na changamoto sana. Hospitali ya Kitete ni hospitali ya rufaa lakini ni hospitali inayohudumia Wilaya mbili; inahudumia Wilaya ya Uyui, inahudumia na Wilaya ya Tabora Manispaa ambazo Wilaya hizi hazina hospitali za Wilaya. Bajeti ya hospitali ya Wilaya ya Tabora Mjini imetengwa lakini bado haijatoka hiyo milioni 500 mwezi huu ninavyozungumza. Angalau Uyui wameshapata na wameanza lakini hospitali ile ya Kitete inapokea wagonjwa wengi kutoka Tabora Manispaa pale pale na wengine wanatokea Uyui.

Mheshimiwa Spika, changamoto inapokuja bajeti ya dawa inayopelekwa hospitali ya Kitete ni ile ile ambayo inapelekwa kwenye hospitali zingine za rufaa bila kuangalia kwamba Kitete inapokea wagonjwa wengi ambao wanatoka kwenye Wilaya ya Tabora na kwenye Wilaya ya Uyui. Kwa hiyo, niombe sana bajeti ya dawa iongezwe katika hospitali yetu ile ya rufaa ili iweze kuendana na mahitaji ya watu wanaohitaji.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusiana na suala zima la Msajili wa Vyama; Msajili wa Vyama majukumu yake yanaeleweka lakini yapo mambo ambayo yanatokea katika Nchi hii hatuoni akiyakemea. Kuna baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa wanatoa kauli ambazo hazipendezi kauli ambazo zinataka kututengenisha, kauli ambazo zinataka kuleta hali ya sintofahamu katika Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiongozi wa Chama cha siasa anapotoka na kujinasibu kwamba yeye anayo Dola, anaweza akatumia Dola ili aweze kupata Dola hii kauli kwa kweli siyo nzuri. Tumekaa muda mrefu hatujasikia majibu yoyote ama neno lolote likitoka kwa Msajili wa Vyama lakini na sisi tumkumbushe Msajili wa Vyama kwamba sisi tunao Wananchi na tunaamini kwamba wananchi hawa watakwenda kutusaidia na sisi tutakwenda kuingia kwenye Dola kama yeye anaamini katika Dola na sisi tunaamini katika wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe sana Msajili wa Vyama vya Siasa atumie nafasi yake kuhakikisha kwamba anatulinda badala ya kutuvuruga. Kama mtu anatoa matamshi iwe ni kwenye Dola, iwe ni sisi huku wa watu wote kila mmoja anatakiwa afuate Sheria na taratibu za Nchi yetu. Kwa hiyo, ningeomba sana hizi kauli zinazotolewa na viongozi wa vyama vya siasa hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi zisiangaliwe tu kwenye vyama vingine hasa vyama vya upinzani lakini viangaliwe hata kwenye Chama Tawala. Hawa viongozi wa Chama Tawala na matamshi yao yanakuaje na yanaathiri namna gani hapo baadaye baada ya uchaguzi mkuu.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka nizungumze kidogo kwenye suala zima la Tume ya Uchaguzi; hizi kelele zinazoendelea za Tume huru, Tume huru, Tume huru nashukuru juzi ulisema kwamba utakaa na sisi pembeni ili tukuambie kwamba hii Tume huru ni nini, nini ambacho kinatakiwa.

SPIKA: Nataka mseme hapa hapa.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA Mheshimiwa Spika, muda hautoshi tuna mambo mengi lakini ni vizuri tukikaa tukakueleza nini hasa tunachokitaka katika kuhitaji hii Tume huru siyo kwamba tunasema lakini tuna mambo ambayo tunayaona kwamba hayaendi sawa katika Tume ya uchaguzi kwa hiyo tunataka yawekwe sawa ili mambo yaweze kwenda sawa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, leo tunakwenda kwenye uchaguzi, wanawake tunakwenda kugombea…

SPIKA: Ahsante sasna, kengele ya pili.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia mapendekezo ya Mpango huu. Naomba pia nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kusimama siku ya leo nikiwa na afya tele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kidogo kwenye sekta ya viwanda. Nilikuwa napitia hapa kwenye sekta ya viwanda; katika ukurasa wa 32, nilikuwa nasoma hapa kati ya mwaka 2015 – 2019, kuna viwanda vipya 8,477 vimeongezeka. Katika viwanda hivyo wameonyesha viwanda vikubwa, viwanda vya kati, viwanda vidogo na viwanda vidogo kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko la ajira katika kipindi cha mpaka mwaka 2015 lilikuwa ni 254,786; lakini 2015 – 2019, ajira zimeongezeka kufikia 482,601. Sasa ukiangalia ukurasa wa 33 Mpango unasema baada ya Serikali kuomba Mifuko ya Hifadhi ya Jamii wameweza kutengeneza viwanda 35 ambavyo katika viwanda hivyo vimetengeneza ajira 250,000. Sasa nataka nifahamu kwanza je, hivi viwanda 35 ni tofauti na viwanda 8,477 na kama siyo tofauti, je, ajira zilizoongezeka ni ngapi? Ni hizi 227,000 zinazoongezeka katika 482,000 ama 250,000 ni ajira tofauti na hizi nyingine na 227,000. Hapa kidogo nimepata changamoto na nikaona bora niulize ili wakati Waziri anakuja ku-wind up atuambie exactly kati ya 2015 - 2019 ni ajira ngapi zimetoka kwa Watanzania kupitia sekta hii ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya viwanda, mwaka 2015 - 2020 ndiyo ilikuwa slogan ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, lakini tunaona ni kwa namna gani bado hatukutimiza lengo ambalo tulikuwa tumekusudia, kama ambavyo mipango ilikuwa ilikuwa inaonyesha. Leo Serikali ilikuwa na viwanda vilivyobinafsishwa na mpango wa Serikali ulikuwa vile viwanda vilivyobinafsishwa kwa wale watu ambao walikuwa hawaviendelezi, viwanda vile vichukuliwe na Serikali. Nilitegemea sasa, baada ya Serikali kuzungumza na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, ingekwenda moja kwa moja kwenye vile viwanda vilivyokuwa na tija wakawapa watu na viwanda vile vikawa havifanyi uzalishaji wangevichukua ili kuendeleza tija iliyokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natolea mfano, Kiwanda cha General Tyre, Serikali ina ubia asilimia mia moja, kiwanda kile ni cha Serikali. Kuna Kiwanda cha Urafiki, kiwanda hiki kilikuwa kinazalisha vizuri sana, demand ya nguo za urafiki huko uraiani ni kubwa kuliko tunavyofikiria. Cha ajabu, Serikali ina ubia wa asilimia 49 na mchina ana ubia wa 51, tuliishauri Serikali hapa kwa nini tusichukue kiwanda kile sisi wenyewe ili tuweze kupata faida, lakini pia kuongeza ajira kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya nyuma Kiwanda cha Urafiki kilikuwa kinaajiri Zaidi, kipindi ambacho hatujaingia ubia na Wachina, lakini tangu tumeingia ubia na Wachina, kiwanda hiki, ajira zimepungua kutoka zilizokuwepo zimepungua kwa asilimia zaidi ya 70. Leo ninapozungumza kiwanda kile haki-operate na hata kama kinafanya kazi walioko pale ni wale viongozi wakubwa tu na kiwanda hiki ni cha kwetu sisi Watanzania, kwa nini tusiwekeze kwenye kiwanda hiki ili kuleta tija kwa sababu tayari Serikali ina ubia wa kutosha katika kiwanda kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuishauri Serikali, viwanda vyote ambavyo tunadhani na tunaona na tunajua kwamba viwanda hivi vilikuwa vinaleta tija kwa Taifa, vinatoa pato kubwa kwa nchi, Serikali iweze kuvirejesha. Hii Mifuko ambayo Serikali inakwenda kuchukua fedha, fedha hizi ni za Watanzania, je, hivi viwanda vilivyowekezwa kuna uhakika gani kwamba, fedha hizi zitarudi kwenye Mifuko kwa wakati ili Watanzania wanaostaafu waweze kupata fedha zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa sana kwa Watanzania wengi katika Mifuko hii kulalamikia mafao yao, lakini leo tumechukua fedha tumekwenda kuwekeza kwenye viwanda 35, lakini kwenye Mpango vinaonyeshwa viwanda vitatu sijui vinne, hatujaonyeshwa hivyo viwanda 35 vyote ambavyo vimewekezwa, lakini tangu uwekezaji umefanyika, je, tumeona kuna tija katika uwekezaji na fedha hizi za Watanzania hawa zitarudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Serikali, badala ya kupelekapeleka tu fedha kwenye maeneo ambayo hayana tija, tuangalie viwanda hivi ambavyo tunaamini vina tija. Leo kiwanda cha General Tyre kifufuliwa nawaambia Watanzania wengi wana magari, tukaamua moja kwa moja hakuna kuagiza matairi kutoka nje, nawaambia hivi, kile kiwanda kitakuwa kina tija, kitaleta ajira, lakini pia kitaongeza mchango mkubwa kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna viwanda ambavyo vilikuwa ni viwanda vya magunia, sasa hivi hata haya magunia ya sulphate ambayo tunatumia wakulima kuweka vitu vyetu wanasema hayafai. Kwa nini viwanda vile visifufuliwe ili magunia yetu ya kizamani yakarudi ili tuweze kupata vifungashio ambavyo vinatakiwa kuliko ilivyo hivi sasa, vifungashio vya sandarusi ambavyo watu wa mazingira wanapiga marufuku. Kiwanda hiki kingefufuliwa kingesaidia kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna Kiwanda cha Nyuzi ambacho kilikuwa katika Mkoa wa Tabora peke yake. Kiwanda hiki ni kiwanda cha muda mrefu. Kilianza kujengwa hata mimi sijazaliwa lakini baada ya hapo kiwanda hiki, baada miaka 10 toka 1975 - 1985 kiwanda hiki kilianza kufanya kazi. Baada ya miaka kumi mwaka 1995, kiwanda hiki kilikufa na kilipewa mwekezaji; mwekezaji huyu ameshindwa kukifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifika pale, Naibu Waziri wa Kilimo kaka yangu Mheshimiwa Bashe alifika pale, waliona hali halisi na ukweli uliopo. Serikali wawekeze kwenye viwanda vyenye tija, Tabora tunalima pamba, Mikoa ya Kanda ya Ziwa inalima pamba, ni rahisi kuchukulika pale na kupeleka Tabora kutengeneza nyuzi zetu kama ilivyokuwa hapo zamani. Ili kuipa uhai TABOTEX Watanzania wa Kanda ya Ziwa na Mkoa wa Tabora waweze kupata ajira lakini Serikali iweze kuongeza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mpango lakini pia mpango bila afya bora hatuwezi kufika. Hapa tumeona Mpango umesema kwamba vifo vya mama wajawazito wakati wa kujifungua vimepungua kutoka 432 hadi 321. Vifo hivi ni vingi sana na vifo hivi vinatokana na umaskini wa wanawake wengi ambao hawana uwezo wa kulipia gharama za matibabu. Vifo hivi ni vifo ambavyo vinajulikana ambavyo vimesajiliwa kwenye hospitali; niambie vifo vinavyotokea kwa watu wanaojifungulia nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi sasa hivi kutokana na gharama ya kujifungua wanawake wengi wameamua kujifungulia nyumbani. Hata hivyo, wanawake wengine wanapokwenda katika hospitali, anapofika maeneo ya hospitali hana uwezo wa kulipia ile hela wakati akisubiri apate msaada wa hela, wanajifungua wakiwa njiani. Hayo tumeyashuhudia na tumeyaona. Kwa hiyo, vifo vya akina mama wajawazito wakati wa kujifungua bado ni vingi, hatuhitaji hii takwimu, tunachohitaji katika Mpango huu vifo viondoke kabisa na siyo kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukizungumza sana kuhusiana na masuala ya afya, elimu na maji lakini miaka 61 ya uhuru wa Tanzania bado tunazungumzia afya, maji na elimu. Hebu ifike mahali tukiwa tunaingia kwenye Mpango hizi biashara ziwe zimeshakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni nchi tajiri ambayo hatupaswi kwa sasa kukaa kuendelea kuzungumzia mipango ya afya. Afya tungesema sasa tunaboresha ama magonjwa ya mlipuko kama Corona na magonjwa mengine yanayotokea ndiyo tungekuwa tunazungumzia sasa lakini siyo afya ya uzazi, mtoto, mama wala ya mwananchi yeyote; hizo zingekuwa ni historia. Toka miaka 61 ya uhuru mpaka leo bado tunazungumzia matatizo ya afya, tuache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya TAMISEMI. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema kwa kunijalia afya na kuniwezesha kusimama hapa na kuchangia hotuba katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili nampongeza Mheshimiwa Waziri Ummy kwa uteuzi. Sina mashaka na utendaji wake, ninaamini kabisa kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu atasimamia Wizara hii sawa sawa ili mambo yaweze kwenda sawa sawa huko chini. (Makofi)

Mheshimwa Naibu Spika, siku zote mazingira bora ya kufundishia na kujifundishia yanategemeana sana na uwepo wa miundombinu rafiki na wezeshi. Hali hii huko chini haipo. Ninaposema hali hii huko chini haipo, ni ukweli usiopingika, miundombinu ya kufundishia siyo rafiki kabisa. Mimi natokea Mkoa wa Tabora ambao ni moja kati ya mikoa iliyoko pembezoni na ni moja kati ya mikoa ambayo ina changamoto kubwa sana za miundombinu ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mkoa wa Tabora ni moja kati ya mikoa mitatu ya juu ambayo inaongoza kwa watoto kupata ujauzito. Hii inatokana na watoto kutembea umbali mrefu kufuata shule zilipo. Vile vile Jimbo la Tabora Mjini ni moja kati ya majimbo ambayo yana changamoto kubwa sana ya Shule za Sekondari. Mtoto anatoka umbali mrefu mno kufuata shule ilipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe mfano wa Kata chache za Tabora Mjini. Kuna Kata ya Kakola ambayo haina kabisa Shule ya Sekondari, haina! Watoto wa Kakola, anatoka Kata ya Kakola umbali wa zaidi ya kimometa 30 kufuata shule kwenye Kata ya Uyui. Anapotembea kutoka Kakola kuja Uyui, siyo kwamba anatembea kwenye barabara, ni pori kwa pori mpaka afike kwenye Kata nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo yanayomsibu mtoto wa kike kwenye maeneo hayo ni mengi sana. Tutalaumu wazazi, lakini mwisho wa siku wazazi pia wanajitahidi kwa kadri inavyowezakana. Naiomba sana Serikali, iangalie uwezekano wa kupeleka Shule za Kata kwenye maeneo ambayo hayana Shule za Kata hasa kweye kata za pembezoni katika Jimbo la Tabora Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule nyingine za Kata ziko katika Kata nyingine. Kwa mfano, Kata ya Gongoni ambayo mimi ndio natokea, Kata ile tunaambiwa kuna shule pale, lakini shule hii iko kule Lwanzari ambako ni Kata ya Ng’ambo. Kwa hiyo, mtoto anapofaulu katika Shule za Kata ya Gongoni anatakiwa moja kwa moja aende Lwanzari, atembee zaidi ya kilomita 20 kufuata Shule ya Sekondari ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii taarifa kwamba kila Kata ina Shule za Sekondari, kwa kweli siyo sahihi. Tatizo hili lipo kwenye kata nyingi. Kata ya Kanyenye; Shule ya Sekondari ya Kata ya Kanyenye inapatikana katika Kata nyingine kabisa ya tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana, Wizara iangalie…

T A A R I F A

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami Mbunge ninayetoka Mkoa wa Tabora. Anasema kutoka Gongoni kwenda Lwanzari ni kilometa 20, hapana, ni kilometa nne. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hawa Mwaifunga unaipokea taarifa hiyo?

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, inategemea na Gongoni sehemu gani? Kwa hiyo, asichukulie Gongoni ya hapa mpaka pale kwamba ni kilomita nne. Kwa hiyo, naomba atulie kwanza, naye ataweza kuchangia kwa nafasi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyopo kwa shule ni kubwa sana. Kata ya Itonjanda katika Jimbo la Tabora Mjini ni kata ambayo ina changamoto kubwa sana ya Shule ya Sekondari. Kuna Shule ya Sekondari moja pale Itonjanda Centre, lakini wazazi wa Kata ile katika Kitongoji cha Kilino waliamua kwa nguvu zao kujenga Shule ya Msingi. Walipata msaada wakajengewa madarasa mawili na ofisi ya mwalimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kujengewa madarasa yale, watoto wa Kitongoji cha Kilino wanasoma darasa la kwanza na la pili peke yake, basi. Ukitaka kumuendeleza mtoto wako madarasa yanayofatia ni lazima uende centre. Kutoka Kilino kwenda pale centre ni umbali mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, wazazi wale waliamua kujichangisha wenyewe, wakaweka mawe, wakanunua na cement. Kwa masikitiko makubwa cement ile imekuwa jiwe, kwa sababu Serikali imeshindwa kuwasaidia kuendelea kujenga madarasa yanayofuata ili watoto wao waweze kupata elimu, ukizingatia kitongoji kile watu wanaoishi kule ni wafugaji wa jamiii ya Kisukuma, walioamua kwa dhati ya moyo wao kwamba watoto wao waende shule, lakini wakisoma darasa la kwanza na pili, biashara imekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie aje aone hilo eneo, aone ni namna gani Wizara inaweza kusaidia watoto wale ili waweze kuendelea na masomo badala ya kuendelea kuwa wafugaji maisha yao yote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule za Tabora Mjini zina zaidi ya watoto 2,000 katika shule moja. Tunaposema elimu bora ndugu zangu, ni pamoja na kuangalia idadi ya watoto katika shule husika. Wakati sisi tukiwa tunasoma; mimi nimesoma Shule ya Msingi Isike, darasa langu lilikuwa na wanafunzi 48 peke yake mpaka namaliza darasa la saba, lakini leo darasa moja lina watoto zaidi ya 100 na kitu. Hii idadi ya watoto 2,000 kwenye hizi Shule za Msingi, ni kipindi ambacho tuko kwenye kampeni, ndiyo idadi hiyo ilikuwepo. Sijui sasa hivi watoto waliosajiliwa kuingia Darasa la Kwanza hali iko namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, miundombinu ya madarasa haipo, siyo rafiki kabisa, watoto wanabanana, watoto wanasoma asubuhi na jioni na elimu ya mchana siyo elimu nzuri hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya kwenye suala la elimu, namwomba sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu atusaidie katika Mkoa wetu wa Tabora katika zile shule 300, naomba sana, chonde chonde, Mheshimwa Waziri atuangalie kwa jicho la tatu Mkoa wa Tabora hasa Halmashauri ya Tabora Mjini ili tuweze na sisi kupata hizo shule ziweze kusaidia wananchi wetu kupata elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye Sekta ya Afya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja ya Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema kwa kunijalia afya tele, nimeweza kusimama hapa tena na kuchangaia hoja ya Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa napenda kumpongeza Kamshna wetu wa Mkoa wa Tabora kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuhakikisha kwamba Wana-Tabora na maeneo mengi wanaweza kufanikiwa kupima ardhi na kupata hati zao. Kamashna huyu ametoa ushirikiano mkubwa kwa Wana-UWATA, yaani Umoja wa Wana-Tabora chini ya Mwenyekiti wetu Bwana Othuman Mahango, amefanya kazi kubwa sana. Leo watu wengi sasa katika Manispaa ya Tabora wana hati zao mikononi ambazo zitawawezesha hata kwenda kupata mikopo katika taasisi mbalimbali za kifedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kwenye zoezi la urasimishaji. Zoezi hili limekuwa na changamoto nyingi sana, pamoja na kwamba linakwenda lakini limekuwa likienda ndivyo sivyo katika maeneo mengi. Tatizo kubwa liko kwenye baadhi ya makampuni haya yaliyopewa kazi ya kufanya zoezi hili. Kwanza wengi makampuni yao hayana uwezo, hayana vifaa na pia wamekuwa hawana wataalam wa kutosha, hivyo kusababisha zoezi hili kuendelea kusuasua na kuwa zoezi ambalo halionyeshi manufaa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa sababu ameliona hili jambo, lakini ameelekeza kwamba angalau haya makampuni yawe yanashirikiana na watendaji katika Halmashauri mbalimbali, lakini kwa masikitiko makubwa, huko ndiko kubaya zaidi kwa makampuni haya, hasa yanayofanya vizuri. Wamekuwa wakidaiwa ten percent sana. Nimwambie Mheshimiwa Waziri, hili linakuwa ni changamoto kubwa sana kwa makampuni haya, inafika mahali wanashindwa kabisa kuelewana na mwisho wa siku hii kazi inakuwa haifanyiki kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishauri Wizara, zoezi hili wanapolitoa kwenye haya makampuni angalau waweke deadline ili basi wakati wanaingia ile mikataba, wawaambie kwamba unapopewa hii kazi wahakikishe mpaka muda fulani kazi hii iwe imeshakamilika. Bila hivyo malalamiko yataendelea kuwa mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wakati wa zoezi hili la urasimishaji tungeiomba sana Wizara ifanye utaratibu wa kuhakikisha wanawafikia wananchi, kuwashawishi na kuwaeleza umuhimu wa zoezi hili la urasimishaji kama ambavyo ilivyofanyika katika Jiji la Mbeya; tumefika pale sisi kama Kamati na tumekuta wamefanyiwa urasilimishaji na hakuna changamoto zozote baina ya wananchi na Wizara. Kwa hiyo, niseme tu kwamba zoezi lile limeenda vizuri; na maeneo mengine Mheshimiwa Waziri tunaomba yafanye hivyo ili kupunguza hizi kele na changamoto ambazo zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tabora ni moja kati ya Mikoa ambayo imezungukwa na mapori mengi ya akiba na hifadhi nyingi. Naomba sana Wizara itusaidie katika mkoa wetu kwenda kuainisha mipaka ya maeneo haya ili kuondoa migogoro baina ya Wizara ya Maliasili na wananchi. Kwa kweli naongea kwa masikitiko makubwa kwa sababu moja kati ya migogoro inayosikitisha ni mgogoro uliopo katika Jimbo la Kaliuwa; mgogoro baina ya Hifadhi pale Isawima na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie, twende katika Jimbo la Kaliuwa akasaidie kuainisha mipaka ili mipaka ya hifadhi ijulikane na mipaka ya mwisho ya wananchi ijulikane ili wananchi wale waweze kuwa na amani pamoja na Askari wa Hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu hizi fedha ambazo Wizara inazitoa kwa Halmashauri mbalimbali kwa ajili ya kupima, kupanga na kurasimisha. Hizi Halmashauri ambazo zimepata fedha ziko Halmshauri zimefanya vizuri na niseme kuwa nazipongeza ikiwepo Halmashauri ya Mbeya Mjini, lakini zipo Halmashauri ambazo zinafanya masihara na hizi fedha, wanadhani kwamba fedha hizi wamepewa kama bakshishi ama za kwao. Fedha hizi Halmashauri mbalimbali zimepewa ili wapime, Halmashauri nyingine zimepima, zimepata fedha na faida juu, lakini wameshindwa kurejesha fedha hizi ili ziweze kusaidia Halmashauri nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Wizara, wakati inataka kutoa fedha hii iangalie uwezo wa hizo Halmashauri husika, ili wazipe fedha Halmashauri ambazo zinaweza kupima na kuuza ili waweze kurejesha fedha na Halmashauri nyingine ziweze kupata fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, huu mradi ni mzuri sana, unasaidia sana kupima maeneo mengi. Serikali kupitia Wizara ya Fedha iweze kuongeza fedha katika eneo hili ili Halmashauri nyingi ziweze kupima na kurejesha fedha na kupata fedha katika Halmashauri zao za kuendeleza upimaji wa siku hadi siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie eneo la National Housing. Kwa masikitiko makubwa, Halmashauri mbalimbali zimekuwa zikiomba kujengewa nyumba za gharama nafuu kwenye maeneo yao, lakini ulipaji wa fedha hizi umekuwa ni wakusuasua na wakukatisha tamaa kabisa. Tumekwenda Momba kweli, tulijionea hali halisi ya zile nyumba, lakini niseme pamoja na kwamba mkataba wao ulikwisha, lakini bado wameendelea kulipa na tumeona bado wana moyo wa kulipa ili waendelee kuzitumia nyumba zile.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kuna Halmashauri nyingine yaani wala hawana hata wasiwasi, kuna wengine National Housing wameamua kuchukua Nyumba zao, wameamua kuzipangisha na mwisho wa siku wamepata hasara tofauti na walivyotegemea, ikiwepo Halmashauri ya Uyui.

Mheshimiwa Naibu Spika, naona Mheshimiwa Naibu Waziri ananikumbusha kwamba Uyui; niseme tu ni ukweli kwamba Halmashauri ya Uyui katika Mkoa wangu wa Tabora na yenyewe ni moja kati ya Halmashauri iliyojengewa nyumba 32, lakini Halmashauri ile imeshindwa kuzilipa, mpaka sasa wamelipa shilingi milioni 200 peke yake katika shilingi bilioni 1.8.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni jambo la kusikitisha sana, lakini naomba nishauri kwenye eneo hili, National Housing kupitia Wizara ya Ardhi wana maeneo mazuri katika maeneo ya Miji, ikiwemo katika Jimbo la Tabora Mjini, wana eneo zuri, liko nyuma pale ya TRA, eneo lile lina miundombinu yote, lina barabara, kuna umeme, kuna maji, yaani hakuna shida kabisa. Waende wakawekeze pale, fedha ipo, haina matatizo yoyote. Vile vile kuna maeneo kama Kawe, Bunda Mjini, Tarime Mjini na maeneo mengine ambayo yanaweza kuuzika kwa hizi nyumba kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa sana naomba nizungumzie suala zima la madeni ya Serikali katika Wizara hii. Ni aibu kuona Serikali inawadai wananchi wa kawaida, taasisi za kawaida mpaka wanafikia kuwapeleka Mahakamani watu hawa kwa sababu ya madeni, lakini Idara, Taasisi na Wizara za Serikali zina madeni makubwa na ya aibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiiuliza Wizara wanakwambia wanashindwa kuwapeleka Mahakamani kwa sababu na hiyo ni Serikali. Ningependa kushauri kwenye eneo hili, kama Wizara inashindwa kuwadai wakiwepo wao wenyewe Wizara ya Ardhi, wanadaiwa zaidi ya shilingi milioni 324, wanatakiwa wazilipe, wanashindwa kuzilipa na wao wana deni, kwa hiyo, ningeomba sana fedha hizi kama inashindikana kwa Serikali kupelekana wenyewe kwa wenyewe Mahakamani, basi watusaidie madeni haya ili yapelekwe CAG na CAG aweze kuziita Wizara hizi na Taasisi za Serikali ili tujue hizi fedha zitaletwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana waweze kutuambia hata Waziri atakapokuja ku-wind-up hapa, atuambie hizi fedha za Serikali zikiwepo kwenye Wizara yake lini zitalipwa? Kwa sababu tunazihitaji hizi fedha, tunahitaji tukapimie watu wetu, tunahitaji hizi fedha kwa matumizi mbalimbali, zilipwe. Watu binafsi wanapelekwa mpaka Mahakamani kwa sababu ya madeni haya, inakuwaje? Wenyewe wa Serikali tuwafanye nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri jambo la mwisho, kumekuwa na Idara ya Mipango Miji katika Wizara hii, lakini bado ujenzi holela umekuwa ukiendelea katika maeneo ya miji mbalimbali. Tungetaka kufahamu idara hii inafanya kazi gani kuzuia ujenzi holela katika maeneo mbalimbali ya miji yetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika bajeti hii ya Serikali. Kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia afya njema, nimeweza kusimama hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeisikia bajeti iliyoletwa na Mheshimiwa Waziri, yapo maeneo ambayo niseme yamefanya vizuri, lakini yapo maeneo ambayo yana changamoto na inabidi zifanyiwe marekebisho kutokana na mapendekezo ya Wabunge na michango ya Wabunge inayoendelea katika Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia kwenye suala zima la wafanyabiashara na TRA, hii imekuwa ni changamoto kubwa sana na ya muda mrefu, kwa wafanyabiashara kugongana na watendaji wa TRA, lakini naamini baada ya kauli ya mama, lakini pia katika bajeti hii inaonyesha sasa wafanyabiashara wanakwenda kufanyabiashara zao kwa utulivu, kwa amani na kwa salama zaidi kuliko ilivyokuwa hapo nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo nyuma ilikuwa mfanyabishara ana wasiwasi na mteja akiingia dukani anajua huyu sijui katumwa, huyu sijui namna gani, lakini mwisho wa siku sasa wafanyabiashara wamekuwa na amani na biashara zinaenda kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii pia imezungumzia maslahi ya wafanyakazi. Kimekuwa ni kilio kikubwa sana kwa Waheshimiwa Wabunage wengi wanaposimama kuhusiana na maslahi ya wafanyakazi. Jambo hili limeonekana na niseme tu bado kuna vitu vidogo ambavyo vikifanyiwa marekebisho naamini kabisa wafanyakazi wetu nao sasa watafanya kazi kwa amani na mambo yao yataenda vizuri kama ambavyo wamekusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Ubunge lakini pia mimi ni mwanamichezo. Niseme tu kwamba Serikali imeondoa kodi kwenye hizi nyasi bandia, lakini kwenye hili naomba niiambie Serikali isiondoe kodi hizi kwenye majiji peke yake kwa sababu ukiangalia majiji yako sita tu na majiji mawili tayari yanavyo viwanja vyenye nyasi bandia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye hili nashauri kwamba, iwe ni kwa nchi nzima kwa sababu mimi natokea Mkoa wa Tabora. Pale katika Mkoa wetu wa Tabora tuna kiwanja chetu cha Ali Hassan Mwinyi, kiwanja kile ni kikubwa, kiwanja kizuri, lakini kimetelekezwa, kimeachwa kwa muda mrefu sana. Ni imani yangu hizi nyasi bandia zikiletwa, angalau na sisi pale Tabora sasa tutaweza kucheza michezo mizuri hata hii michezo ya ligi kuu itakuwa inaletwa katika uwanja wetu pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe tu na nishauri kwa Serikali, utaratibu wa vibali basi wawape BMT ili waweze ku-control uagizaji wa nyasi hizi hili kusiwe na vurugu ya hapa na pale ya wafanyabiashara kutaka kuweka mambo yao mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kuishauri Serikali, hizi fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika maeneo yetu tungeomba sana zisiwe kwenye makaratasi. Fedha hizi ziende ziende zikafanye kazi ambazo zimekusudiwa. Leo mimi hapa ninavyozungumza katika Mkoa wetu wa Tabora tumeletewa maji ya Ziwa Victoria. Maji yamefika lakini bado hayajasambazwa kwa wananchi, kwa hiyo niombe sana fedha hizi zipelekwe ili ile miradi ambayo inahudumia wananchi wengi iweze kufanyika, baada ya bajeti hii watu waweze kupata ile huduma ambayo inatakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kama ambavyo tumeshauri kwenye bajeti za Wizara mbalimbali kuna masuala ya zahanati, Vituo vya Afya, hospitali za wilaya kwenye wilaya ambazo hatuna hospitali za wilaya, tungeomba sana fedha hizi ziende na zikawe kipaumbele ili wananchi wetu waweze kupata huduma bora kama ambavyo mama amepanga na anataka huduma hizi zifanyike hasa huko chini zikiwepo huduma za afya, elimu na maji. Kwa hiyo naomba sana fedha hizi zisiwe kwenye makaratasi za kufurahisha watu lakini ziende sasa zikafanye utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la ushirikishwaji wa Wabunge wa Viti Maalum katika fedha zinazopelekwa za miradi ya maendeleo kwenye maeneo yetu. Wabunge wa Viti Maalum tumekuwa vinara wakubwa wa kueleza changamoto zinazotukabili katika mikoa yetu na maeneo yetu. Kama unavyofahamu sisi Wabunge wa Viti Maalum tunatumikia mikoa sio majimbo peke yake na tunapozungumza hapa tunazungumzia mikoa yetu na sio majimbo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo changamoto zinazoletwa katika Bunge zinapokelewa, zinachukuliwa, katika utekelezaji wake Wabunge wa Viti Maalum tunawekwa pembeni. Juzi zimepelekwa shilingi milioni 500 kwenye kila jimbo, Wabunge wa viti maalum hatujashirikishwa. Juzi nimemsikia wifi yangu Ummy Mwalimu akizungumzia kuhusiana na fedha zitakazokwenda kujenga mashule, katika majimbo. Mheshimiwa Ummy amesema kwamba watakaa na Wabunge wa Majimbo ili waweze kuona ni kata zipi ambazo zitakwenda kupeleka hizo shule.

Sisi wanawake wa Viti Maalum tumeshiriki kwa namna moja ama nyingine kuzungumzia changamoto zilizopo za mashule, tunaomba tushirikishwa na sisi hili tuweze kusema kwamba wapi shule hizi ziweze kupelekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkoa wangu una majimbo 12 Wabunge wa viti maalum tupo watatu inashindikana nini kutuingiza kwenye hizo fedha hili na sisi tuweze kushiriki katika fedha hizi za maendeleo ambazo tunazipigania hapa Bungeni. Jambo hili kwa kweli linaumiza na niseme tu linaonyesha kwamba kama Wabunge wa Viti Maalum hatuna chochote ambacho tunatakiwa kukipata. Wabunge wa majimbo wana fedha za majimbo wanapata, wanafanya kazi, Wabunge wa majimbo miradi ya maendeleo inayokwenda wanapewa inakwenda kufanya kazi, sisi Wabunge wa Viti Maalum tunatumia fedha zetu wenyewe kufanya majukumu yetu na kutekeleza majukumu yenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinapofika kipindi cha kampeni, Wabunge hawa wa majimbo wanatutegemea sana sisi Wabunge wa Viti Maalum tuwasaidie kwenye kampeni ndio wanashinda majimbo hayo. Wasituogope tunakwenda kufanya kazi pamoja ili tuweze kuleta maendeleo katika maeneo yetu. Naiomba sana Serikali, sisi ni Wabunge, tunaomba itushirikishe na sisi tunahitaji kufanya maendeleo katika maeneo tunayotoka na ndio maana tumekuwa tukichangia sana kuhakikisha kwamba maeneo yetu, barabara, miundombinu ya hospitali, shule na kila kitu tunaizungumzia hapa. Kwa hiyo ningeomba sana tushirikishwe, fedha za maendeleo zinapokwenda na sisi tuwe ni sehemu ya fedha hizo kwa sababu tunaziombea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nikizungumzia sana kuhusiana na sekta ya viwanda kipindi cha bajeti za nyuma. Niseme tu kwamba, bado tuna changamoto kubwa sana katika sekta hii. Bado ni baadhi ya viwanda vichache tu ambavyo vinaweza kutoa kodi kubwa kwa Serikali tofauti na ambavyo tunaambiwa viwanda vilivyo vingi. Kwa hiyo ningeiomba Serikali na kuishauri kuangalia namna bora ya kuwezesha viwanda hivi ili viweze kuwa na tija katika Taifa letu kwa kuongeza kipato cha Taifa letu kwa maana ya kuongeza pia kodi za makusanyo ya kila mwaka katika nchi yetu. Naomba sana sekta hii ya viwanda iangaliwe vizuri, kwani ni sekta kubwa ambayo inaweza ikawa na mchango mkubwa sana katika pato la Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee kidogo suala zima la sekta ya utalii. Zipo changamoto kidogo katika sekta hii. Ni sekta ambayo Serikali inategemea kuleta kodi na kipato kwa Serikali, lakini ina changamoto kubwa sana katika maeneo mbalimbali ya hifadhi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto za miundombinu katika baadhi ya hifadhi zetu. Hiyo inapelekea kukwamisha watalii wengi kuweza kufika katika maeneo yetu. Bado tuna changamoto pia ya kuona ni namna gani tunavyoweza kuboresha maeneo yetu ya utalii kwa ujumla yaweze kuendana na hali halisi ambavyo watu wanaisikia Tanzania na utalii jinsi ilivyo. Kwa hiyo, naomba sana katika bajeti hii tuweze kuboresha kwenye sekta hii ya utalii ili basi sekta hii iweze kuongeza pato zaidi ambalo limekuwa likipatikana kwani sekta hii inategemewa sana na nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia mpango huu wa mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuaji wowote wa uchumi katika nchi yoyote unategemea mipango thabiti ambayo mmejiwekea kama Taifa. Siku za nyuma kidogo kulikuwa na filamu ya Royal Tour. Tumeona ni kwa namna gani mafanikio makubwa ya filamu ya Royal Tour yanakuja katika nchi yetu, lakini kama Taifa tumejiandaa namna gani kukabiliana na wimbi la wageni ambalo litakuja katika nchi yetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mipango au katika mpango huu sijaona sehemu yoyote ikisisitiza kwamba kama Taifa tunategemea kuongeza mapato yetu kupitia utalii. Utalii kwa Tanzania unakua kwa kasi ya hali ya juu, lakini mpaka sasa kama Taifa tunategemea kupata mapato ya asilimia 17 tu kutoka katika suala zima la utalii. Tuna uwezekano mkubwa sana wa kuongeza mapato yetu kupitia sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo vitu vingi sana, tuna vivutio vingi sana, tuna mambo mengi sana katika nchi hii ambayo tukiyatangaza tukiyaweka vizuri katika Taifa letu haki ya Mungu utalii utakuwa unaongoza kwa zaidi ya asilimia Thelathini katika mapato ya Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na hifadhi 16, leo tunapozungumza Tanzania tuna hifadhi 22. Hifadhi hizi 22 bado kama Taifa hatujaona umuhimu wa kutengeneza mpango madhubuti wa kuhakikisha hifadhi zote hizi angalau hata nusu ya hifadhi hizi zinaingiza kipato cha kutosha. Leo ninapozungumza na Bunge hili ni kwamba, bado watalii wanapokuja kwenye nchi yetu, wanatamani kwenda Serengeti na Zanzibar, lakini tunahifadhi na vivutio vingi kweli kweli ambavyo watalii hawa ama wananchi wa Tanzania ambao wanapenda kwenda kutalii wakitangaziwa nchi hii itakuwa inaongoza kwa mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Wizara haitakuwa na mpango madhubuti wa kuhakikisha kwamba inaongeza bajeti kwenye sekta hii ya utalii tutaendelea kupiga mark time na badada ya hii asilimia 17 tutashuka asilimia 15 mpaka asilimia 10 kwa sababu hatuko serious kwenye jambo hili la utalii. Shida yetu ni kwamba tunagusa kila kitu hatuangalii zile sekta muhimu ambazo zinaweza zikifufua uchumi wetu na uchumi ukapaa ukawa mkubwa kuliko ilivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo hifadhi ya TANAPA ambayo inasimamia hizi hifadhi 22, lakini bajeti waliyonayo tangu wanasimamia hifadhi 16 mpaka leo ni ileile Bilioni 1.5 wanaendelea kuwa nayo mpaka leo. Hivi kutoka hifadhi 16 mpaka leo 22, bajeti ni ileile hivi kweli tuko serious, tunataka utalii wa nchi hii ukue? Ningeomba sana katika mpango huu ambao tunakwenda kwa ajili ya kuandaa bajeti, hebu watuletee bajeti ya maana katika Wizara hii ya Maliasili ili tuweze kukuza utalii wetu. Tunahitaji kuwa na asilimia za kutosha katika sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusiana na suala la Bandari Kavu. Mimi ninatokea Mkoa wa Tabora, Mkoa wa Tabora ni eneo ambalo reli ya SGR inapita. Kama ulivyoona hata katika sensa Tabora ni moja kati ya Mikoa mikubwa sana na ina maeneo makubwa sana, mimi ningeomba Serikali iache kigugumizi wapeleke Bandari Kavu katika Mkoa wa Tabora. Watakapopeleka Bandari Kavu katika Mkoa wa Tabora sisi tutafanya biashara na nchi za Maziwa Makuu kwa urahisi zaidi. Ukitoka Tabora kwenda Katavi, Mpanda na Kigoma ni rahisi kuliko maeneo mengine yoyote na tutaweza kufanya biashara na nchi Mbili mpaka Tatu kwa pamoja, kuliko ambavyo sasa hivi kumekuwa na kigugumizi tunataka huku tunataka huku. Serikali ifanye maamuzi katika Mpango mnaokuja nao, tengeni fedha ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kujenga Bandari Kavu katika Mkoa wa Tabora na kama kuna nia thabiti ya kuinua Mikoa ya pembezoni basi fanyeni hili. (Makofi)

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti,taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kumpa taarifa mchangiaji Mheshimiwa Hawa Mwaifunga Dada yangu kuwa Serikali ya Mkoa wa Tabora chini ya Mkuu wetu wa Mkoa Mheshimiwa Batilda Burian umeshatenga eneo kwa ajili ya kujenga Bandari Kavu hii ambapo Serikali ikiwa tayari basi watapatiwa eneo. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru kwa taarifa yake maana kutenga ni jambo moja lakini utekelezaji ni jambo lingine. Kwa hiyo, hapa tunachofanya ni kuhakikisha kwamba tunasisitiza kwa sababu tayari kumeshakuwa na mvutano, Mkoa wa Tabora tayari umeshatoa heka zaidi ya 1,000 bila fidia yoyote. Kwa hiyo, mimi ninaomba sana Mheshimiwa Waziri tusaidieni hii Mikoa ya pembezoni inahitaji kuendelea, ili tuweze kuendelea na wananchi wetu waweze kuwa na mafanikio katika uchumi wao tunaomba sana mtusaidie, hii Bandari kavu itakapokuja pale Tabora itasaidia sana wananchi wetu pia itasaidia kukuza uchumi wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie upande wa Kilimo, ni ukweli usiopingika kwamba Mikoa mingi inalima mazao ya biashara lakini sisi ambao tunatoka Mkoa wa Tabora zao kubwa la biashara ambalo tulikuwa tunalitegemea wakati wote ni zao la Tumbaku. Tabora ni Mkoa ambao umeonekana kwamba unao uwezo wa kulima mazao mengi ya biashara na yakastawi vizuri. Tabora tunalima alizeti, korosho, tumbaku, mahindi, maharagwe na kadhalika. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa kazi kubwa ambayo anaifanya nasi tunamuahidi kumpa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha kwamba nchi yetu tunakwenda kuingia kwenye kilimo cha kisasa badala ya kutegemea zaidi mvua na jembe la mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono suala zima la block farming, lakini ninaiomba Serikali iliangalie hili jambo kwa jicho la tatu, iwe ni lazima kwenye kila Mkoa na Wilaya kutengwe maeneo kwa ajili ya hizi block farming ili wananchi wetu waweze kunufaika na kilimo kwenye suala zima la block farming. Kama Tabora tunao uwezo wa kulima korosho, lakini wanapotokea wateule wakasema kwamba hatuwezi kulima korosho kwa sababu yataharibu zao la asali. Mimi nimezaliwa Tabora nimekua Tabora, lakini sijawahi kuona tajiri wa asali zaidi ya watu wanaovuna asali hela wanayopata ni kwa ajili ya watoto kusoma, chakula na mambo mengine madogo madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kwenda mbali zaidi ili kuweza kuwasaidia wananchi wetu wawe na tija. Kwa mfano, likija zao la korosho baada ya miaka mitano au kumi watu wakaanza kuvuna korosho, Mkoa ule utabadilika na mwisho wa siku watu wetu wakawa matajiri na kufanya kazi kubwa. Kwa hiyo, ninaomba sana kupitia mipango hii kwenye suala zima la kilimo tusaidiane kuhakikisha kwamba angalau hawa wateule, kila mteule ajue kwamba katika Mikoa hii tuweke hizi block farming na katika Wilaya hizi ambazo tunaweza kuweka basi iweze kufanyika hivyo, ikiwepo Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tena nizungumzie suala zima la afya. Wakati nikipitia mpango nimeona kwamba wanazungumzia suala zima la kupunguza vifo vya watoto na mama wajawazito, lakini hizi takwimu zinasema sahihi? Je, hizi takwimu si ni zile ambazo zinakuwa recorded vipi kuhusu zile takwimu ambazo haziko recorded? Wanawake wengi sana wanajifungulia nyumbani na barabarani. Je, hawa nao takwimu zao tayari zinakuwa zimeshaorodheshwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza kwamba vifo viumepungua kwa asilimia hizi lazima tuwe na uhakika wa kuona hata kwenye yale maeneo ambayo wanawake wengi wanajifungulia majumbani na barabarani taarifa zake zinakuwa recorded na zinapelekwa na zinakuwa taarifa sahihi ili tuweze kujiridhisha na kuona kwamba ni ukweli kama Taifa tumepunguza vifo vya mama na mtoto, kuliko hivi sasa tunazungumza vitu kinadharia na vitu vile ambavyo tunaviona viko pale lakini kiuhalisia siyo sahihi. Kwa sababu sisi tunaotoka kwenye maeneo ya vijijini ambayo ni mbali na hospitali tumeshakutana na kadhia hizo nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta Mama ameshajifungua, wameshamfanyia kila kitu pale kamaliza biashara, lakini saa zingine unaweza kuta mtoto amepata athari au amekufa ama mama amekufa taarifa hizo hazitoki. Kwa hiyo, mimi niombe sana kama Wizara katika mpango wenu muangalie na muone namna gani ambavyo mnaweza kujua kwamba wanawake wangapi kwa mwaka wanakufa katika nchi hii kwa ajili ya uzazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja ya Wizara hii ya Mawasiliano. Kwanza nikupongeze kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge na leo umekalia kiti hicho. Naomba Mwenyezi Mungu akuongoze uendelee kuwa na hekima kama ilivyokuwa hapo awali tuendelee kwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na malalamiko makubwa sana ya masuala ya ma-bundle. Wananchi wengi sana wamekuwa wakilalamikia wizi mkubwa unaofanywa katika ma-bundle. Unapoweka bundle unapewa expire date, unaambiwa kwamba hii utatumia kwa mwezi mmoja, utatumia kwa wiki moja, utatumia kwa siku moja, lakini unaweza usitumie kwa mwezi mmoja, lakini inapofika ule wakati wanakufyeka inabidi uweke fedha nyingine sasa fedha hizi zinakwenda wapi? Tungeomba sana Wizara ya Mawasiliano waangalie jambo hili, limekuwa likipigiwa kelele sana na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walichofanya wamerudisha vifurushi vile ambavyo gharama ambazo zilikuwa hapo zamani. lakini, bado kuna hitaji kubwa sana la wananchi kutumia vifurushi hivi, lakini gharama hizi zinaonekana ni kubwa hasa kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Waziri anawasilisha hapa amezungumzia kuhusiana na masuala mazima ya kesi za wahalifu wa mitandaoni. Mheshimiwa Waziri hajatuambia mpaka sasa, ni kesi ngapi mpaka sasa zimeshatolewa maamuzi. Kwanza zipo ngapi, lakini ni ngapi mpaka sasa zimeshatolewa maamuzi. Pia ni adhabu gani zinazochukuliwa kwa watu hawa wanaohusishwa na uhalifu wa mitandaoni. Labda wakisema wazi pengine haya mambo yanaweza yakapungua kulingana na adhabu ambazo zinatolewa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya TCRA kufungia Vyombo vya Habari bila kuwaita na kuwasikiliza. Tunataka kujua, haki iko wapi kama unamfungia mtu bila kumsikiliza. Malalamiko yamekuwa makuwa hasa kwa hawa wanaotumia mitandao ambao vyombo vyao vya habari viko mitandaoni. Wanafungiwa sana bila hata kuitwa na kusikilizwa na wao waweze kujieleza. Kwa hiyo, ningeomba sana Serikali iwe inafanya utaratibu wa kuwaita wale wanaowafungia, wawasikilize, wakishawasikiliza ndiyo waweze kufanya maamuzi kuliko kuwaumiza kama ambavyo wanafanya sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na ufungiaji pia wa vyombo vya habari kama magazeti na magazeti haya yamekuwa yakichaguliwa, yapi yafungiwe na mengine yasifungiwe. Sasa tungetaka kujua, Serikali ituambie ni utaratibu upi au ni maudhui gani yanayotakiwa kwenye gazeti yaandikwe ndiyo gazeti lifungiwe na gazeti hili lisifungiwe. Kwa sababu unaona kuna magazeti mengine yanaandika vitu vya ajabu lakini utashangaa magazeti haya hayafungiwi, yanafungiwa magazeti mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba tufahamu na tujue haya magazeti yanayofungiwa, yanafungiwa kwa makosa yapi na haya ambayo yanaendelea kuwepo na tunayaona mitaani yakiandika vhabari za ajabu, yenyewe yanakuwa na uhalali gani wa kuendelea kuwepo kwenye tasnia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba nishauri kidogo Serikali kuhusiana na suala zima la ruzuku. Ningeishauri Serikali iondoe mpango wa kutoa ruzuku kwa watoa huduma za internet ili kupunguza gharama za upakuaji wa mada ama machapisho ama vitabu. Tunafahamu kabisa sasa hivi hata wanafunzi wanapewa masomo yao katika mitandao. Sasa wanapokuja kwenye suala la kupakua unakuta kwamba gharama inakuwa kubwa zaidi. Kwa hiyo, nashauri Serikali ingejitahidi kutoa ruzuku ili basi wanafunzi hawa na hata maeneo mengine ya watu wa Serikalini ambao wanafanya machapisho mbalimbali ziweze kuwa hazina gharama zozote, yaani iondolewe kabisa na iweze kuwa bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoka Mkoa wa Tabora. Moja kati ya Mikoa ambayo ina changamoto kubwa sana ya mawasiliano, unaweza ukajikuta umetembea hatua chache tu huwezi kupata mawasiliano. Amezungumza hapa Mbunge wa Tabora Mjini lakini naomba niongezee. Jimbo la Tabora Mjini lina Kata 29, katika kata hizi 29, Kata 12 ni Kata za Vijijini. Unapokwenda kwenye Kata hizi, ukitoka tu kwenye kata ya mjini ukaingia kwenye kata ya vijijini mawasiliano yanakata kabisa. Kwa hiyo, hata kama unakuwa na changamoto yoyote ambayo umeiacha huku mjini, mtu anapokutafuta huwezi kupata mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Wizara iangalie maeneo haya iweze kutupelekea minara ili wananchi wale na wao waweze kupata huduma ya mawasiliano. Kwa sababu, inafika mahali mtu anapotaka kupata mawasiliano lazima apande kwenye eneo la muinuko…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ya pili hiyo, ahsante na mwinuko.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ya kwanza!

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia nkatika hoja zilizowasilishwa. Kwanza ningependa kuunga mkono hoja ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii ambayo ni kamati ninaihudumu kwa kipindi hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tuliiomba na tunaendelea kuomba kama kamati kuona namna bora ya kuweza kuongeza fedha katika mashirika ambayo yanahudumiwa na Wizara hii ya Maliasili ikiwepo Shirika la TANAPA lakini pia TAWA. Kumekuwa na uongezaji wa hifadhi lakini pia kumekuwa na uongezaji wa mapori. Yote haya yanahitaji kuhudumiwa, kwa mfano leo tunavyozungumza TAWA wameongezewa mapori matano zaidi kutoka mapori 22 yamekwenda kuwa mapori 27. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapowapa mapori mengine zaidi kwa bajeti ile ile hawa watu wanakwenda kufanya kazi namna gani? Tunaona jinsi ambavyo kuna changamoto, wanyama wakali wanakwenda kuvamia watu, kuvamia mashamba ya watu, hawa watu hawana manpower ya kutosha, hawana fedha za kutosha, tunategemea hawa watu wafanye kazi kwenye mazingira gani? Niiombe sana Serikali iweze kutenga fedha ya kutosha ili hawa watu waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tunaiangalia TANAPA. Tukiangalia pia kwenye suala zima la utalii, hawa watu wanakusanya mapato, TFS halikadhalika wanakusanya mapato. Mapato yale yanapokusanywa sasa hivi yanakwenda moja kwa moja kwenye mfuko mkuu. Kutoka kwenye mfuko mkuu kurudi huku imekuwa changamoto. Niiombe Serikali itambue kwamba ukitaka kula sharti uliwe. Toa fedha upate fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapotaka kupata fedha bila kutoa fedha utapata wapi? Toeni fedha watu wafanye kazi fedha ziingie. Mheshimiwa Waziri wa Fedha tunaliomba sana hili jambo ili mfuko wako uweze kutuna zaidi wape watu fedha wanaoingiza fedha. TANAPA wanaingiza mapato, TFS wanaingiza mapato, TAWA wanaingiza mapato lakini yale yanapoingia hayarudi hawa watu waende wakafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa tunapozungumza Royal Tour imelipa, wageni wanakuja chungu nzima, hawa watu wanaumiza vichwa hawa wageni watakaokuja kwenye hii high season safari hii wataenda kulala wapi? Watakwenda kulala wapi kwa sababu hawana fedha ya kuweza kuendeleza mipango mingine ya kuhakikisha wanaendelea kupokea wageni. Mpaka kuna wakati kamati tulishauri labda pengine tuliwahi sana kutangaza hii Royal Tour wakati bado Serikali hamjajiandaa. Hebu tuwe serious na haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tunataka utalii uweze kuongeza mapato katika nchi hii ni lazima tufike mahali tukubali kupoteza fedha ili tupate fedha kwa sababu tunahitaji fedha. Vinginevyo tutapiga mark time tutalaumu watendaji, tutalaumu Waziri, tutabadilisha mawaziri lakini mwisho wa siku bila fedha hii Wizara haiwezi kufanya kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali, nimuombe Waziri wa Fedha aiangalie hii Wizara kwa jicho la tatu, aiangalie kwa umakini mkubwa, ahakikishe kwenye haya mashirika wanaongezewa fedha ama wanarudishiwa hata ile incentive angalau kwa 20% ili hawa watu waweze kufanya kazi. Wame-stuck, wamekwama. OC zenyewe sasa hivi zinachelewa, hawa watu wanafanyaje kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana kwa upande wa maliasili niombe sana kwenye bajeti waongezewe bajeti. TAWA mpaka leo tangu mwaka 2018/2019/2020 wanapewa shilingi bilioni 45 pekeyake, niambie na bado mnaendelea kuwaongezea mapori. Hawa watu wanafanyaje kazi? Lazima fedha ziongezwe ili watu waweze kufanya kazi kwa ufanisi ili mambo yaweze kwenda vizuri kama tunataka kutangaza utalii wetu na kufanya utalii ndiyo uwe unaongoza katika pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kwenye upande wa ardhi. Ardhi ni changamoto sana nchini kwetu, siyo siri kama utakumbuka bajeti iliyopita watu walizungumza sana kuhusiana na masuala mazima ya ardhi lakini pia waliiomba Serikali kuona namna bora ya kuongezea tume ya matumizi bora ya ardhi fedha ili waweze kupanga matumizi ya ardhi kwa sababu kupanga ndiyo kila kitu katika ardhi ya Tanzania. Tukishapanga ardhi hii tukapima vijiji vyetu sawasawa, matatizo na changamoto za ardhi zitakuwa ni story. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema na ninarudia tena labda kama matatizo ya ardhi kwenye Serikali imekuwa ni mtaji, pengine labda itakuwa ni hivyo lakini kama tunahitaji mwarobaini, ni lazima tukubali kuweka fedha katika tume ili tume hii iweze kufanya kazi yake kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliomba fedha hapa bajeti iliyopita, tuliomba shilingi bilioni 10 wakakosa wakaongezewa shilingi bilioni nne katika shilingi bilioni moja waliyokuwa wamepewa. Hiyo shilingi bilioni nne hata kwenye bajeti ya safari hii nusu mwaka haijaonekana kabisa lakini ukiuliza unaambiwa Wizara ya Fedha hawajatoa, yaani wanafanya kurushiana mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuelewi tatizo ni nini, tatizo ni nani, tatizo ni Wizara ya Fedha, Wizara ya Ardhi watatuambia hapa kwamba tujue kwamba matatizo na changamoto za ardhi ni mitaji kwao, watuambie hapa kwamba sisi matatizo ya ardhi ndiyo mitaji yetu kwa hiyo mtuache ili tuendelee na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kamati tulitegemea Wizara ya Ardhi imepata mkopo nadhani mtaiona humo kwenye taarifa yetu ya kamati. Mkopo wa zaidi ya shilingi bilioni 345. Tukategemea katika mkopo huo japokuwa kamati tulikuwa hatujui habari ya mkopo huo wala tulikuwa hatujui nini kinaenda kufanyika, walipotuletea tukagundua katika shilingi bilioni 345, shilingi bilioni 345, vijiji vinavyokwenda kupangwa ni vijiji 250 pekeyake katika vijiji zaidi ya 9000 ambavyo vinatakiwa vipangwe, vipimwe na viwekwe katika mpango mzima wa matumizi bora ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bilioni 300, wakati tume ya upangaji wa ardhi waliomba shilingi bilioni 10 waende wakapime vijiji 600 kwa mwaka lakini leo tumepata fedha za mkopo ambazo Watanzania watakwenda kuzilipa hizi fedha, leo ndani ya miaka mitano Wizara inakwenda kupima vijiji 250 bila aibu halafu fedha nyingine zote zinapelekwa kwenye seminar wamejitengea five bilion, bilioni tano imetengwa kwa ajili ya seminar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamejitengea uratibu, yaani kwenda kuratibu kwenye hayo maeneo wanayokwenda, wametenga zaidi ya shilingi bilioni 40, zitakwenda kutumika kwa ajili ya kazi hiyo, kuna uboreshaji wa ofisi za Wizara, kuna ujenzi wa ofisi kwenye kila mkoa, mikoa 25 wameweka fedha hizi. Kuna matengenezo ya magari wameweka fedha hizi, kama Mbunge niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu mkopo huu tuombe tuupitie kwanza. Huu mkopo ndugu zangu mikopo ina maneno mengi huko nje, Mheshimiwa Rais anatembea kila kukicha asubuhi, saa sita na jioni kutafuta fedha, hizi fedha kama hazina tija kwa Watanzania, hazina tija kwa wananchi, huu mkopo utatu- cost. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa kuna taarifa ya Mheshimiwa Waziri.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, atajibu si Waziri? (Kicheko)

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Angelina.

T A A R I F A

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nataka kumpa taarifa tu msemaji na bahati nzuri ni mjumbe wa kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapochukua mkopo au unapoingia mkataba wowote unakuwa una lengo lake. Lengo la mkopo huu uliochukuliwa, lengo kuu ilikuwa ni kuweka miundombinu ya kujenga mifumo, kujenga uwezo wa wataalam, kununua vitendea kazi ili kazi ya upangaji na upimaji iweze kukamilika vizuri na iwe endelevu, ndiyo lengo la mkopo. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa taarifa hiyo.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mabula ni Mbunge wa CCM, ilani ya chama chao inasemaje ndani ya miaka mitano kupima vijiji vingapi? Lazima tunapochukua fedha tuchukue fedha kwa malengo na mipango ya nchi na Taifa kwa ujumla lakini pia fuata ilani ya chama. Inakwambia nini? Ufanye nini ndani ya miaka yako mitano? Haiwezekani hata kama mna malengo mchukue shilingi bilioni tano muende mkafanye seminar na watu wanaokwenda kuseminishwa ni hao hao wafanyakazi wa ofisini kwao ambao tayari wanajua mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nchi hii haina tatizo la mfumo. Leo Serikali ilitoa fedha kwa ajili ya mfumo wa ILMIS. Umefanya kazi Dodoma na Dar es Salaam, niambie mpaka leo nenda pale Dodoma, ni shida na changamoto kubwa. Mfumo umeshindwa kufanya kazi. Mfumo unafanya kazi.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa, Mheshimiwa Ole Sendeka karibu.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani mnanitoa kwenye stimu.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge anayeongea. Nimepata habari kwamba yeye ni mjumbe wa kamati hiyo na kwa maelezo ambayo ameyasema na maelezo ambayo Mheshimiwa Waziri ameyatoa. Kama hali iko hivyo ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameeleza na fedha hizo zinakwenda katika mazingira ya aina hiyo ya kusema kujenga uwezo na posho hizo zinakwenda katika mazingira hayo, Serikali nashauri itoe maelezo kwa sababu naunga mkono hoja anayoizungumza Mheshimiwa Mbunge. Hatuwezi kuwa na matatizo ya upimaji wa maeneo halafu fedha zote zinakwenda kwenye Wizara. Maelezo yatolewe kwenye Bunge hili.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa unaipokea hiyo taarifa?

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake kwa mikono miwili. Kwa sababu kama Waheshimiwa Wabunge, tutakubali huu mkopo uende ukafanye kazi ya haya ambayo wameyaandika kwenye taarifa, naomba msome taarifa ya kamati. Haya yamo na wamechanganua naomba msome taarifa ya kamati. Kama tunakwenda kukubali haya, hali ilivyo huko nje watu wanavyopiga kelele na mikopo, leo tunakwenda kukopa fedha, tunakwenda kupima vijiji 250 katika vijiji 9,000 ambavyo vimebaki havijapimwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu uhuru nchi hii imepima vijiji 2,600 peke yake. Katika vijiji 12,000 na ushee tumepima vijiji 2,600 peke yake. Halafu vipaumbele vyetu ni nini kwenye suala zima la ardhi? Vipaumbele vyetu ni kujenga ofisi za Wizara? Vipaumbele vyetu ni kulipana posho? Kutengeneza magari? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani, huu mkopo uangaliwe upya, upitiwe upya ili wakati tunakwenda mwaka 2025, vijiji vyote 9,000 vilivyobaki vipimwe, hii fedha ni nyingi itolewe shilingi bilioni 145 vijiji vipimwe, wakati Mheshimiwa Rais anakwenda kumnadi, hili nalo liwe ni sehemu ya kampeni zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Wizara hii ya Afya. Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama tena kwenye Bunge hili nikichangia katika Wizara hii ya Afya.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri kwa Serikali kupitia Wizara hii ya Afya. Kumekuwa na ujenzi wa hospitali za Wilaya, kumekuwa na ujenzi wa vituo vya afya, kumekuwa na ujenzi wa zahanati nyingi sana ambazo ukipita kwenye Halmashauri mbalimbali hospitali hizi za Wilaya hazifanyi kazi, vituo vingi vya afya havifanyi kazi, zahanati nyingi hazifanyi kazi kwa sababu hazina vifaatiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi niombe sana, nafikiri kwamba hii kasi ya Mheshimiwa Rais anayoenda nayo ya kuweka miundombinu ya afya muende nayo na nyinyi sasa Wizara ya Afya kwa kupeleka vifaatiba pamoja na Madaktari na Wauguzi katika hospitali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi ukizunugumza kwamba kuna hospitali za Wilaya, kuna vituo vingi vya afya kama havifanyi kazi, wananchi hawa hawawezi kuona tija ya hivyo vituo vya afya na hizo hospitali za Wilaya ambazo zinajengwa. Kwa hiyo, niombe sana kupitia Bunge lako Tukufu, Wizara hii sasa ijikite zaidi katika kupeleka vifaatiba, kupeleka Madaktari pamoja na Wauguzi ili majengo haya yaweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, majengo ni mengi mno tumeyaona na tumeshuhudia lakini hayana vifaatiba wala hayana Madaktari, maeneo mengine yanavyo vifaatiba lakini hayana wataalam. Unafika unakuta mitambo imefungwa hapo, iko vizuri imekaa sawa sawa hakuna wataalam. Unauliza huu mtambo umefungwa lini? Una mwaka mzima hakuna mtaalam, huu mtambo umefungwa lini? Una miezi sita hakuna mtaalam.

Mheshimiwa Spika, tumekwenda Halmashauri ya Sumbawanga Mjini kuna kifaa kipo zaidi ya miaka miwili sasa hakijawahi kufanyakazi wala kufunguliwa kule kwenye makaratasi. Sasa hii ni kitu gani? Mimi naomba tuwe tunaangalia zaidi vipaumbele vyetu hasa kwenye afya ni kitu gani ili tuweze kusaidia wananchi wetu, tuendane sawa na kasi ambayo anakwenda nayo Mama ya kuhakikisha kwamba watu wanapata huduma za afya, basi huduma za afya zipatikane kwa tija inayohitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala zima la dawa. Mheshimiwa Waziri amekuwa mara nyingi sana hapa akizungumzia suala la dawa, kwamba sasa hivi hakuna shida ya dawa. Inawezekana hakuna shida ya dawa lakini dawa zinazotakiwa katika maeneo yale ndiyo zinazokosekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unakuta kuna hospitali haina panadol, unashangaa mbona Waziri kasema pale kuna madawa, hata panadol kweli hakuna? Lakini utakuta kuna dawa zinawekwa kwenye hospitali husika hazina hata watumiaji mpaka zina expire. Kwa nini tusiangalie uhitaji wa dawa zinazohitajika kwenye hospitali zetu na kwenye maeneo yetu ili tupeleke zile dawa zinazohitajika, wananchi waweze kupata huduma ya dawa kuliko ilivyo hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetembea kwenye hospitali mbalimbali tumekuta dawa zime-expire ziko pembeni zinatakiwa zitupwe lakini ukiwauliza naomba paracetamol hakuna, naomba cetirizine hakuna. Sasa tunaomba sana muangalie ni dawa gani ambazo zinahitajika kuchukuliwa ili wananchi wetu waweze kupata huduma inayostahiki kuliko ilivyo hivi sasa kupeleka tu dawa bora mmepeleka dawa mwisho wa siku dawa zile hazifanyi kazi na matokeo yake zinaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuzungumzia kuhusiana na suala zima la maradhi haya ya kansa. Hili jambo limekuwa ni janga tena ni janga kubwa sana hasa kwetu sisi wakina mama. Kansa hasa za shingo ya kizazi zimekuwa ni nyingi mno, kiasi kwamba mwanamke mpaka uje ujigundue kwamba una kansa ya kizazi hasa wanawake wetu wa maeneo yetu ya vijijini kupima ni kwa nadra. Unakuta imeshafika stage ambayo haiwezekani tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi natokea Mkoa wa Tabora. Katika Mkoa wetu wakina mama wengi sana wanapata matatizo hayo, mwisho wa siku anapopata tatizo hili hana pa kwenda kukimbilia, anaambiwa aende Bugando ama aje hapa Benjamini Mkapa. Ni wangapi ambao wanao uwezo wa kufika kwenye maeneo hayo? Kwa hiyo, unakuta mama huyo mpaka tayari stage yake imefika mbaya anaelekea kufa unaweza ukamsaidia lakini unamsaidia wakati tayari hali imeshakuwa mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana, kwanza elimu inahitajika sana hasa kwa wanawake wetu maeneo ya vijijini kuhusiana na hili janga. Sisi wa mjini angalau tunajua kama nitakwenda hospitalini naomba mni-check, mni-check matiti, mni-check na kizazi nitaangaliwa na nitakutwa labda niko salama ama nina dalili za huo ugonjwa lakini wenzetu kule ni ngumu sana. Kwa hiyo, niombe sana Wizara ya Afya mfanye kazi ya ziada tusaidie wanawake hawa wanakufa sana, pamoja na hizo tezi dume zinazosemwa lakini kwa kweli kansa za wakina mama zimekithiri sana maeneo mbalimbali katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana tupelekewe na sisi basi hivi vifaatiba vya kansa pale katika Hospitali yetu ya Kitete katika bajeti hii, tunawaomba jamani mtusaidie. Hawa wanawake tuweze kuwaponya ili angalau na wao sasa waweze kupata nafuu na kujua kwamba wanapata huduma ile maeneo yale.

Mheshimiwa Spika, Tabora imefunguka, barabara sasa hivi zimefunguka, kila sehemu magari yanapita yanaingia. Tusaidieni basi ili angalau watu wa kutoka hata kwenye Wilaya za karibu waweze kufika pale kwenye hospitali yetu ya Kitete waweze kupata huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nifahamu kuhusiana na suala la Bima ya Afya hasa kwa Watoto, imekuwa kero kubwa sana. Hatuelewi, hatujui tushike wapi. Ukiwauliza wanakwambia, kuna siku nilimuuliza Naibu Waziri akaniambia inabidi mzazi amsajili na mtoto wake kwenye bima yake. Mimi mtoto wangu ameshakuwa mkubwa lakini kuna watu ambao wana watoto wana miaka mitano. Huyu mtoto analipa wapi na bima yake imesha-expire? Hebu tunaomba Mheshimiwa Waziri unapokuja hapa, utoe majibu yatakayowaridhisha wananchi huko waweze kujua, mtoto wa kuanzia mwaka mmoja mpaka mitano ambaye bima yake imesha-expire anatakiwa afanye nini ili aweze kupata bima ya afya? Kwa sababu ukisema ni shule, shule gani anasoma mtoto huyu, kwamba labda ataenda kusajiliwa shuleni? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba mtoe maelezo basi yatakayowasaidia huko wazazi wengi, au kama ni kulipa hiyo shilingi 190,000 semeni. Mzazi lipa shilingi 190,000 mtoto wako aweze kupata huduma ya afya vieleweke kuliko kuwa mnafumba fumba na kusema kwamba watu wote wasajilini watoto kwenye mashule yao. Shule gani wengine watoto wadogo bado hawaja anza hata hizo shule? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind up hapa, atupe majibu ya kuhusiana na hili suala la bima ya afya hasa kwa hawa watoto wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na madeni pia makubwa sana katika Wizara hii ambapo hospitali nyingi sana za Kanda na hospitali za Mikoa zina madeni yaliyokithiri. Niombe sana Wizara ya Fedha pelekeni fedha wenzenu waweze kulipa madeni haya. Saa zingine kuna huduma nyingine zinakwama kwa sababu ya madeni makubwa ambayo wanayo katika hospitali zetu za Kanda na hospitali zetu za Mikoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya CAG ya Hesabu za Serikali Kuu ya mwezi Machi, 2023, Wizara ya Afya ina madai ya zaidi ya shilingi bilioni 9.21. Madai hayo yanadaiwa katika hospitali ya Rufaa ya Apollo. Inaonekana kwamba kuna baadhi ya wenzetu Serikalini wanatibiwa huko, kwa hiyo kuna madeni hayo ambayo yanadaiwa kwa mujibu wa Taarifa ya CAG ya Machi, 2023 muende mkaipitie muione. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hospitali zetu 33 za Rufaa na za Mikoa kuna madeni ya jumla ya zaidi ya shilingi bilioni 34.02. Hizi fedha ni nyingi sana na hapa hata ukizitoa, haya ni madeni ya muda mrefu zaidi ya miezi 12 madeni haya wala hayana mpango wa kulipika.

Mheshimiwa Spika, nitoe tu mfano wa hospitali chache hata hii hospitali yetu mnasema Mirembe mimi najua bado Mirembe sijajua kama tayari imeshabadilishwa lakini ina deni la zaidi ya shilingi bilioni tatu. Kuna Hospitali ya Kanda ya Mbeya ina zaidi ya deni la shilingi bilioni tatu. Dodoma hapo hospitali ya General zaidi ya shilingi bilioni 2.8. Hata hospitali ya Mkoa wa Tabora Kitete ina zaidi ya deni la shilingi milioni 948. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaiomba Wizara ya Fedha iweze kusaidia haya madeni kuondoka ili watu waweze kupata huduma zinazostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona umeshika mic naona muda wangu umeisha. Nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama hapa na mimi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ningependa niipongeze Kamati ya Kudumu ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa hotuba nzuri sana ambayo wameiwasilisha katika Bunge hili na nipende kusema jambo moja Wabunge tunapochangia tuangalie Kamati yetu imetuelekeza wapi kwa sababu hawa wenzetu ndio wanaojua mambo yote yanayoendelea katika wizara hii kwa sababu ndio wanaofanya nao kazi wakati wote. Kwa hiyo, tunavyotaka kuishauri na kuisimamia Serikali tujaribu kuangalia wenzetu wamesema nini? Kamati ndio Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najaribu kupitia taarifa ya Kamati ya Bunge na nimeona ni kwa namna gani ambavyo Wabunge wenzetu wameweza kuchanganua na kufafanua yale yote ambayo waliyoyasema katika hotuba aliyosoma Mwenyekiti. Nikupongeze sana Mwenyekiti wa Kamati hii ndugu yangu Mnzava kwa kazi nzuri na kubwa uliyoifanya na wajumbe wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa kwenye Kamati hii kwa kipindi cha miaka miwili na nusu ninaijua vizuri sana, na ninaamini yale uliyoyaandika siyo majungu ndio ukweli uliopo na uhalisia na unachofanya ni kuisaidia Serikali ili iweze kutekeleza majukumu yake, ili iweze kuondoa migogoro inayowasumbua Watanzania kwenye maeneo yetu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za ardhi katika nchi yetu ni nyingi sana na kila siku ni afadhali ya jana, unapomuona Mbunge anasimama anazungumza kwa uchungu anajua ni namna gani wananchi wake wanapata adha na shida kubwa ya ardhi. Tunapozungumzia suala la kupanga matumizi bora ya ardhi siyo kwa sababu tuna kitu tunachokitaka zaidi ya kwamba tuondoe migogoro kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inayo Tume na nimwambie Mheshimiwa Waziri ana Tume nzuri sana, ina watendaji wazuri kweli kweli, hawa watu wakipewa mshiko, wakipewa fedha wanaenda kufanya kazi kweli kweli. Mimi hapa leo ninavyozungumza katika Mkoa wangu wa Tabora fedha kidogo walizopewa wameshakwenda kwenye vijiji zaidi ya 16 mpaka sasa ninavyozungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Tume, tulikuwa na mgogoro mkubwa sana wa vijiji katika Jimbo la Igalula, Kata ya Kizenga kuna vijiji viwili mgogoro umedumu pale kwa zaidi ya miaka nane, lakini wamekwenda juzi wamemaliza mgogoro ule kwa sababu ulikuwa kila siku unawafanya watu wanafungwa, unawafanya watu wanapelekwa mahabusu bila sababu zozote. Mimi ninavyozungumza hapa Mwenyekiti wangu wa Kijiji wa wakati huo mwaka 2017 aliwekwa ndani kwa sababu ya mgogoro huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie Mheshimiwa Waziri na Wizara yake asifikiri Wabunge wanaposimama na kuzungumza masuala ya kupanga matumizi bora ya ardhi tunazungumza tu, lakini tumeona na tunajua faida ya kutoa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yetu tumechoka kufiwa kwa sababu ya migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wanalia kila leo kwa ajili migogoro ya watu wanauana na mimi nafikiri na nilisema hii migogoro huenda inanufaisha Wizara kwa namna moja ama nyingine, kuna manufaa wenzetu ambayo wanayapata kwa sababu haiwezekani kama hakuna manufaa wasisikilize haya ambayo tunasema na wanayaona na wanayajua, lazima wafike mahali wajue kwamba migogoro ya ardhi inachosha na niwaambie niwakumbushe tu...

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Nimemuona Mheshimiwa Waziri.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri atajibu anamaliza muda.

MWENYEKITI: Naomba upokee Taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, karibu.

TAARIFA

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Hawa siyo kwamba namaliza muda.

Ninakushukuru sana na ninakupongeza kwa kuisifia Tume kwa kumaliza huo mgogoro, ili kusaidia Bunge hili lijue kwamba Wizara ya Ardhi haina manufaa yoyote na migogoro hiyo Tume inafanya kazi chini ya Wizara ya Ardhi, kwa hiyo kama unaona kuna mafanikio yoyote yamepatikana kupitia kwenye hiyo Tume ni kwa sababu Wizara ya Ardhi imeisimamia vizuri Tume, ni kwa sababu ya Serikali imeisimamia vizuri Tume. Kwa hiyo, naomba nikupe tu taarifa kwamba hivyo vitu vyote ni taasisi za Kiserikali na ni Serikali inayofanya hiyo kazi nzuri kwa pamoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwaifunga, unapokea taarifa?

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti,...

MWENYEKITI: Mheshimiwa sijakuruhusu.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anhaa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, unapokea taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi?

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, amenielewa Dada Jenista na anachokisema ina maana anakubaliana na mimi, migogoro ikiondolewa ina maana migogoro ikiondolewa hawa wa Tume wakipewa fedha ina maana hakutakuwa na mazingira yoyote ya watu wetu kufa kwenye maeneo yetu na ndichi hiki ambacho nimekisema kwamba inawezekana kuna baadhi ya migogoro inawanufaisha na hili silifuti ndio ukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa sana kwa baadhi ya Makamishna ambao wako kwenye mikoa yetu mbalimbali. Mimi nimpongeze Kamishna wa Ardhi amefanya kazi kubwa sana, amechukua ushauri vizuri sana wa Kamati, tulimuomba Mheshimiwa Kamishna atusaidie labda kufanya rotation ya hawa Makamishna inaweza ikasaidia kwa kiasi fulani kupunguza migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimekuwa na Kamishna katika mkoa wangu wa Tabora tunamshukuru sana amefanya kazi kubwa sana, sasa hivi kuna maeneo kwa kweli husikii migogoro, Wabunge sasa hivi kuna maeneo tumepumzika kusikiliza migogoro Kamishna aliyekuwepo, lakini hata huyu aliyeletwa sasa ninaona anaendeleza kazi ambayo imefanywa na mwenzake aliyetangulia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna maeneo mengi yana migogoro ukiwepo Mkoa wa Dodoma, Dodoma yaani ni kasheshe. Kwa hiyo mimi nimuombe sana Mheshimiwa Waziri hawa Makamishna mliowafanyia rotation, wapeni muda waweze kufanya kazi, waweze kuonesha kile ambacho mnakitaka sasa, kama mmeamua kupata mabadiliko kwenye Wizara kupitia hawa Makamishna, wapeni muda, wapeni ushirikiano waweze kufanya kazi ili muweze kuona matunda yao, mkiweka au kuhamisha watu bila kuangalia kwa nini mnawahamisha mnaharibu na matokeo yake huyu anamlaumu huyu na huyu anamlaumu huyu, mwisho wa siku migogoro inakuwa haipungui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba na nizungumze kidogo kuhusiana na hili suala la hii fedha ya mkopo na Kamati imefafanua vizuri sana. Mikopo tunapokwenda kukopa Serikali ninyi mnakwenda kwa niaba yetu sisi Watanzania kwa sababu mwisho wa siku hamlipi ninyi hiyo mikopo ni sisi Watanzania tunalipa kupitia kodi zetu. Sasa kama unapewa mkopo una masharti ambayo unayaona hayana manufaa kwa Watanzania una sababu gani ya kuchukua mkopo huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichukua mkopo hapa wa trilioni 1.3; Mheshimiwa Rais alipata huu mkopo na masharti ya mkopo huu ilikuwa tununue barakoa na sanitizer. Trilioni 1.3 Mheshimiwa Rais aliona hivi trilioni 1.3 naenda kununua barakoa na sanitizer wakati kuna watoto wanakaa chini, wakati kuna watoto wanasoma chini ya miti, wakati kuna wanawake wanajifungulia majumbani, wanawake wanajifungua barabarani, kwa nini mkopo usiwe wa kuweza kusaidia Watanzania kule walipo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mkopo wa trilioni 1.3 tumeona manufaa yake, kila unapokwenda kwenye majimbo kuna madarasa yamejengwa, kila unapokwenda kwenye majimbo yetu kuna zahanati na vituo vya afya vimejengwa, leo tunapozungumza hapa tunalalamikia vitu vidogo vidogo, siyo majengo tena, je, mama angechukua huu mkopo akaenda kununua sanitizer na barakoa tungekuwa tunagaragara nazo tu hapa Bungeni kwa sababu hazina kazi, corona imeshakwisha au kama bado ipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkopo wa trilioni 1.3 fedha ya uratibu iliyotumika, monitoring and evaluation hawa walitumia bilioni tano tu, katika trilioni 1.3 walitumia bilioni tano peke yake, lakini wenzetu wamechukua bilioni 345 uratibu peke yake wanatumia zaidi ya bilioni 47, hatukatai kwamba wanaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Watanzania wanauana kwa sababu ya ardhi nani atakwenda kwenye Ofisi za Ardhi hizo ambazo mnataka kuzijenga? Leo mnachukua fedha eti mnaenda kununua furniture, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge niwambie leo tunapokaa tunazungumza hapa Watanzania wanatuangalia na wanatuona, mwaka 2025 is around the corner, hakuna mtu atakayekuja kukusaidia kwenye jimbo lako utapambana mwenyewe. Mheshimiwa Jenista kakaa pale ataenda Peramiho, mimi nitakuwa Tabora hakuna atakaye kuja kunisaidia lazima nipambane na hali yangu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema huu mkopo lazima uangaliwe ili uendane na tija kwa ajili ya Watanzania na si vinginevyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii. Kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia uhai na afya tele nimeweza kusimama hapa muda huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ningependa kuzungumzia utekelezaji wa bajeti ya maendeleo katika Wizara hii kwa miaka mitatu iliyopita. Utekelezaji wa bajeti ya maendeleo katika Wizara hii umekuwa hafifu mno kwa miaka mitatu iliyopita. Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya 2018/2019 fedha za miradi ya maendeleo hadi kufikia mwezi Machi, 2019 zilikuwa zimepelekwa kwa asilimia 16 peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019/2020, na haya sio maneno yangu yapo kwenye randama za Wizara ya Afya za miaka hii mitatu, fedha zilizotengwa zilikuwa jumla ya shilingi bilioni 544.137 lakini hadi kufikia mwezi Machi mwaka 2020 kiasi cha fedha kilichokuwa kimetolewa ni shilingi bilioni 83.06 peke yake sawa na asilimia 15.3 tu. Mwaka 2020/2021 bajeti iliyotengwa ilikuwa ni kiasi cha shilingi bilioni 360.9 lakini mpaka mwezi Machi mwaka 2021, mwaka huu, fedha zilizokuwa zimepelekwa ni shilingi bilioni 83.1 peke yake. Kwa hiyo, utaona ni kwa namna gani fedha zinatengwa lakini haziendi kutekeleza yale ambayo tumekubaliana katika Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii inaonesha kwa miaka yote mitatu fedha zimekuwa zikipelekwa angalao kwa asilimia 18 tu kila mwaka. Sasa uone ni namna gani changamoto za afya zinavyozidi kujitokeza kwasababu, fedha zile zilizokusudiwa haziendi kama ambavyo tumezipangia bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kubwa sana katika maeneo yetu. Mimi natokea Mkoa wa Tabora, Jimbo la Tabora Mjini; kuna suala la wanawake kwenda kujifungua na kulipa gharama. Unapojifungua mtoto wa kiume utalipa 50,000/= na unapojifungua mtoto wa kike utalipa 40,000/=. Hili jambo lipo katika hospitali za Mkoa wa Tabora, ikiwepo Hospitali ya Kitete ya Rufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hata juzi hivi ninavyozungumza kuna ndugu yangu katoka kujifungua, amelipa 50,000. Sasa huyo amejifungua mtoto wa kiume, sasa huyo ana uwezo wa kulipa hiyo 50,000/= lakini kuna mwananchi mwingine wa kawaida ambaye uchungu umempata, anakwenda hospitali hana hiyo fedha ya kulipa, vifo vinatokea. Na hii sio uwongo ndio ukweli uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ningeomba sana Serikali atakapokuja kwenye majumuisho Mheshimiwa Waziri aje na majibu, hii ni sheria? Ni utaratibu? Ama ni waraka wa Wizara uliokwenda kwenye baadhi ya hospitali wanatakiwa wachangie fedha hizi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwasababu hata sisi wawakilishi wa wananchi tukihoji tunaambiwa hay ani maelekezo. Sasa tunataka tujue hayo ni maelekezo kutoka wapi? Mheshimiwa Waziri aje aseme hapa, ili wananchi wa Tabora wapate kupona kwasababu hii imekuwa kero kubwa sana katika Jimbo la Tabora Mjini na Mkoa mzima wa Tabora. Na ninaamini kabisa kuna baadhi ya mikoa mingine fedha hizi wanalipa wakati wanawake wanakwenda kujifungua. Hii ni kero kubwa sana kwa wananchi wa Jimbo la Tabora na Mkoa mzima wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tabora Mjini hatuna hospitali ya wilaya, lakini tuna kituo cha afya. Kituo hiki cha afya hakina vifaa tiba, hakina wauguzi, hakina madaktari, hakina dawa. Hivyo, inasababisha wananchi wa Jimbo la Tabora Mjini wengi kwenda kusongamana katika Hospitali ya Rufaa ya Kitete na hivyo kusababisha msongamano kuwa mkubwa zaidi kwa sababu, ile ni hospitali ya rufaa. Sasa tunaiomba sana Serikali iweze kusaidia kituo kile cha afya, tunaomba mkakiboreshe, muweze kuweka vitu kwa ajili ya wanawake kujifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu anatoka kwenye Kata kwa mfano ya Ikomwa, Ikomwa ni kata ambayo iko mbali sana na pale maili tano. Kwa hiyo, mtu anatoka pale anafika pale maili tano anaambiwa dawa hakuna, anaambiwa hakuna vipimo, anaambiwa hakuna, kwa hiyo, mwananchi anajikuta amechoka kwelikweli kiasi kwamba, anakuwa hana jinsi inabidi arudi jinsi ilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba sana Serikali itusaidie iende ikaboreshe kile kituo cha afya. Mnafahamu kabisa Jimbo la Tabora Mjini limegawanyika katika sehemu mbili, kuna kata za mjini kuna kata za vijijini na kituo cha afya kinachotegemewa ni hicho kilichopo maili tano. Sasa tungeomba kama Wizara kuna uwezekano basi tuongezewe vituo vya afya, ili angalao viendane na maeneo ambayo tupo kwasababu, maeneo mengi yako pembezoni na ni makubwa mno na kuna wananchi wanaishi kule, lakini wanapata changamoto kubwa sana ya huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kule kwenye maeneo mengine ya kata za pembezoni hakuna hata zahanati. Watu wanateseka, watu wanapata shida kwelikweli kwasababu ya ukosefu wa huduma za afya. Ningeiomba sana Serikali iuangalie mkoa wa Tabora, iangalie Jimbo la Tabora Mjini tuna changamoto kubwa sana katika huduma za afya. Na haya niliyokueleza ni changamoto ambazo zinatukabili siku hadi siku. Hasa hasa pia, hata hii Hospitali yenyewe ya Kitete ambayo nimezungumza haina vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2018/2019, bajeti ilitengwa hapa kwa ajili ya kufanya ukarabati kwenye vituo vya wazee. Pale Tabora tunacho Kituo cha Wazee Ipuli, kwa kweli kinahitaji ukarabati. Tunahitaji kuwasaidia wale wazee ili na wao angalau waweze kuishi kama wapo sehemu ambapo wanalelewa na Serikali. Kwa hiyo, naomba sana zile fedha ambazo zilitengwa na kama zilikuwa hazijafika basi wajitahidi kuweza kuboresha vituo hivi ili viweze kutunza vizuri wale wazee kama ambavyo Serikali tumekusudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Wizara hii ya TAMISEMI na Serikali za Mitaa. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, kanijalia afya na nimeweza kusimama hapa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye Halmashauri yangu. Mimi ni Diwani kwenye Halmashauri ya Tabora Manispaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuzungumzia kuhusiana na suala la wamachinga. Hili ninalizungumza kwa sababu natamani sana kuwekwe utaratibu mzuri kuhusiana na suala zima la Wamachinga. Kwa sababu pale Tabora Mjini kilichotokea kwa kweli siyo kitendo cha kiungwana. Wamachinga wale wamevunjiwa vibanda vyao tena usiku wa manane, wao wenyewe wakiwa wamelala hawana Habari, asubuhi wanakuja wanakuta vibanda vyao vimevunjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafahamu kabisa Mheshimiwa Waziri atakuwa na taarifa hii, lakini naomba nitoe ombi kwa Mheshimiwa Waziri, kama bajeti yake itakuwa imepita hapa, namwomba sana aende Tabora. Nenda Tabora ukapate uhalisia wa jambo hili, ukapate ukweli wa jambo hili, usisikilize tu peke yake watendaji wako, nenda kawasikilize na wananchi shida iko wapi? Ni kweli wametengewa eneo, lakini eneo lile ni dogo. Je, watendaji hawa wamefanya tathmini ya kujua Wamachinga ni wangapi katika Manispaa ya Tabora? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mahali walipojenga wametenga eneo la watu 500 peke yake. Tabora Mjini haina Wamachinga 500 peke yake, wapo zaidi. Pia nenda kawape watendaji wako elimu, Wamachinga ni watu gani? Kwa sababu wao wanachochukulia, Wamachinga ni wale wanaouza bidhaa tu peke yake za kawaida, lakini hawa akinamama ntilie, wamama wa mbogamboga, wamama wa matunda, wamama wanaopika chapati, mandazi, wanasema wale sio Wamachinga, sasa wale ukiwakuta barabarani unawafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, watoe mwongozo kwenye Halmashauri zetu, kama ambavyo leo tuko hapa, eneo la Wamachinga linajengwa tena kwa ustadi mkubwa na kila kitu…

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Halima Mdee, taarifa.

T A A R I F A

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba changamoto za Tabora Manispaa ziko pia Jimbo la Kawe maeneo ya Tegeta, Magwepande na Bunju. Kwa hiyo, nakupa taarifa ili Waziri adake akijua akitoka Tabora Manispaa aende na Jimbo la Kawe kuna shida kubwa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwaifunga unapokea taarifa?

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo kwa sababu ni ukweli usiopingika kwamba dhana ya Wamachinga inaonekana viongozi wetu huko chini hawaielewi. Ndiyo maana unakuta kumekuwa na changamoto kubwa sana kiasi kwamba, kunakuwa hakuna maelewano baina ya wananchi pamoja na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ukichukuliwa utaratibu kama uliofanyika maeneo ya Morogoro; leo hapa Dodoma Wamachinga tunapita tunakutana nao mitaani, wanasubiri eneo lao special. Wale wakishagawiwa ukimkuta barabarani yule kweli unaweza ukapambana naye; lakini unaenda kupambana na mtu ambaye hata eneo la kufanyia biashara hujampa, unategemea huyu mtu anakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba sana na namwomba sana Mheshimiwa Waziri, nenda mwenyewe kashuhudie hali halisi, vinginevyo hali ya Tabora Manispaa itakuwa haieleweki. Hali ni tete, wananchi mitaji yao imekufa kwa sababu wamevunjiwa wakati wakiwa wamelala na hawana walichokiokoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala zima la afya. Kuna Sera ya Zahanati Kijiji kwa Kijiji. Hii sera inaonekana kwamba haitekelezwi ipasavyo. Katika Jimbo la Tabora Mjini lina kata za mjini na kata za vijijini. Katika Kata za vijijini unakuta kuna zahanati moja peke yake katika Kijiji ambacho kina vitongoji vitano ama sita.

Kwa hiyo, mtu kutoka Kitongoji kimoja kwenda Kitongoji kingine anatembea zaidi ya urefu wa kilometa tano mpaka kumi kufuata hiyo zahanati. Kwa hiyo, naomba sana, hii sera ya zahanati vijiji vyote, naomba iweze kutekelezwa. Pia mliiweka hata kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, tunawaomba sana mtusaidie ili wananchi wetu wa vijijini nao waweze kunufaika na sera hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kata moja ya Isevya; ile Kata ina watu wengi sana. Kutokana na watu wengi sana, pale kuna zahanati. Tulikuwa tunaomba sisi wakazi wa Tabora, kikiwekwa kituo cha afya pale kitaweza kusaidia wananchi wa kata za karibu kuweza kufika pale, kwa sababu pale wanazalisha mpaka watu watano mpaka tisa kwa siku. Nafahamu Mheshimiwa Waziri taarifa hii anayo, naomba utusaidie, tupelekeeni fedha mtuwekee kituo cha afya na pale ili na kile kingine kilichopo maili tano kiweze kusaidia wananchi wa eneo la kata za mjini, ili wawezze kupata huduma sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusiana na masuala ya elimu. Kwenye suala la elimu kumepelekwa fedha nyingi sana katika ujenzi wa shule hasa za sekondari, lakini shule za msingi zimesahaulika kabisa. Pale Tabora Mjini kuna shule kongwe, kama Shule ya Isike, Shule ya Msingi Gongon na Shule ya Msingi Kitete. Shule hizi ni kongwe na zimekuwa ni za zamani sana. Leo imefika mahali mabati yanavuja, mvua zikinyesha yale madarasa wanafunzi hawaingii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chonde chonde, Waziri mwenye dhamana tunaomba mtusaidie, hizi shule za zamani mtusaidie kuzifanyia ukarabati. Nazungumzia shule za msingi, lakini pia msaidie kuongeza madarasa kwenye hizi shule ili wananchi wengi ambao wanaishi maeneo ya mjini watoto wao waweze kupata elimu karibu na maeneo ambayo wanakaa kuliko ilivyo hivi sasa mtoto anatoka umbali mrefu kufuata shule wakati kuna shule ambazo unaweza ukajenga madarasa na zinaweza zikasaidia watoto wetu kusoma karibu na maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri sana ambayo ameiwasilisha ndani ya Bunge letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la tathmini zinazofanywa na baadhi ya watendaji kwa vitisho kwa wananchi wetu. Hivi karibuni, mwaka jana 2022 kwenye suala hili la ujenzi wa Reli ya SGR, route tatu katika Mkoa wetu wa Tabora. Jana niliuliza hapa swali la nyongeza kuhusiana na malipo yao, lakini wakati naliuliza nilisema, pamoja na fedha kidogo ambayo wameambiwa watalipwa lakini bado fedha hii imecheleweshwa kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona leo nilizungumze jambo hili ili liweze kuwekwa sawa. Watendaji hawa walipofika kufanya tathmini ya maeneo ya wananchi wetu hususan katika Manispaa ya Tabora, Eneo la Ndevelwa, watu hawa wamepimiwa maeneo yao, square mita zilizopatikana eti kila square mita moja Shilingi 800. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dunia ya sasa, nchi yetu hii sasa kuna ardhi unaweza kununua square mita kwa Shilingi 800? Hawa watu wana hati, wamesajiliwa, wanajulikana, ni maeneo ambayo ni mapya, hawakukataa kupisha mradi huu kwa sababu ya uzalendo wao. Walisema mradi huu upitishwe, tunahitaji maendeleo ya Wana-Tabora lakini walipwe stahiki zao sahihi. Kwa akili ya kawaida haiwezekani, mtu mwenye square mita 500 anakwenda kulipa shilingi 400,000 wakati leo ukiigusa ardhi Tabora Mjini, huna milioni mbili hupati eneo la kujenga nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu unaenda kumlipa shilingi 400,000 aipeleke wapi? Kwa nini tunataka kuifanya Serikali ionekane haijali wananchi wake, na hasa kwa kipindi hiki ambacho Mama Samia anaongoza ambaye ni mwanamke mwenzetu? Hatutaki jambo hilo litokee, lakini naomba niliseme, tena nalisema kwa machungu makubwa na kwa ukali. Haiwezekani, na kwenye nchi hii na kwenye Taifa hili kuwalipa watu shilingi 800 kwa square mita moja, haiwezekani Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Ofisi ya Waziri Mkuu, jambo hili Mheshimiwa Waziri Jenista na watu wako, tunaomba mwasaidie wananchi wetu ni masikini. Haiwezekani, nendeni mkaone mjue. Tunaumia sisi viongozi wao. Unamlipa mtu shilingi 800! Cha kusikitisha, ninao mfano mmoja hapa, kuna mtu mmoja kalipwa shilingi 350 kwa square mita moja. Huyu mwananchi ana square mita 4,643. Huo ni ukubwa wa eneo lake. Malipo alioyoandikiwa kulipwa, bado hawajalipwa maana yake, hapa nazungumza ni zaidi ya mwaka sasa umepita bado malipo hayo hawajalipwa, atalipwa shilingi 1,639,050. Hayo ni malipo ya fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye kila square mita moja ukipiga hesabu na humu ndani kuna wanamahesabu, kila square mita moja ni Shilingi 350/=. Jamani, sisi watu wa Tabora ni wapole sana, ni wastaarabu, ni wakarimu, lakini msichukulie advantage upole wetu na ustaarabu wetu kutufanyia haya. Yanaumiza! Hivi leo maeneo haya yangekuwa ni yetu sisi viongozi, tungekubali kweli kulipwa kiasi hiki! Mtu ana hati tayari, mtu ana kila kitu tayari ameshaweka pale, anasubiri mji upangwe ili aweze kufanya maendeleo yake kwenye eneo lake! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi umepita mkubwa tumekubali, lakini leo inakuwa ni dhahama sasa! Badala ya raha ya kusema kwamba nataka mradi upite, wananchi wananung’unika, wanasikitika, tutapata wapi baraka? Hii ni dhuluma, siyo haki. Ni lazima Serikali iangalie jambo hili jamani. Hata kama haliwezekani, liangalieni jambo hili mwasaidie hawa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mheshimiwa Mwakibete amelifuatilia jambo hili angalau hiyo amount ndogo ambayo wameandikiwa, Mheshimiwa Mwakibete ameisimamia angalau walipwe kwanza, kama kuna mambo mengine yatafuata. Waheshimiwa Waziri ninyi ni viongozi wenzetu, ni wazazi, mna ndugu, mna jamaa, na marafiki, kwa fedha hii tunaomba watusaidie tafadhali watu hawa waweze kulipwa stahiki zao kwa mujibu wa eneo na maeneo yao. Shilingi 800/= haiwezi kutosha. Yaani kwa kweli naongea kwa uchungu mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusiana na hili suala zima la shule kongwe. Hili suala la shule kongwe limekuwa linazungumzwa tu juu juu. Sisi wananchi wa Tabora tunazo shule maarufu kongwe Tabora Mjini pale. Kuna Shule ya Tabora Boys, kuna Shule ya Tabora Girls. Shule hizi zimetoa watu maarufu na wengine wamo humu ndani. Wengine ni viongozi wakubwa kwenye Taifa hili, lakini kizuri zaidi, Shule ya Tabora Boys Baba wa Taifa, amesoma pale. Ukiona shule zile na hali iliyopo ni aibu hata kusema shule hii amesoma Baba wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali inatuambia tutoe fedha za mapato ya ndani kwenda kufanya ukarabati wa shule hizi, jamani mnatuonea! Hebu saidieni shule hizi za kihistoria ziweze kuwa shule bora. Unapofika pale Tabora, unasema naenda Tabora Boys, hilo geti lenyewe linavyokuitikia, aibu! Halina hata mvuto! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipo kwenye Kamati ya LAAC, tumepita juzi pale. Tunashukuru wafadhili wametusaidia kutengeneza mabweni, wameyakarabati. Tumeingia mpaka chumba cha Baba wa Taifa alicholala, tumekiona, lakini nenda kwenye bwalo, nenda kwenye majengo mengine, ni aibu! Shule ya Tabora Girls kuna watoto wetu wa kike, hata fence tu haina. Wanaume wakware wanapita pale na magari yao kujionesha, kufanyaje, wanawakonyeza watoto wetu, wanawaharabia masomo yao. Wajengewe angalau fence pale kwanza ili watoto wetu waweze kusoma kwa amani na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa dakika chache ulizonipatia. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja hii ya Wizara ya TAMISEMI. Kiukweli niseme tu kwamba nilikuwa najaribu kupitia pitia taarifa ya Mheshimiwa Waziri, lakini mengi niliyokuwa nikiyapitia sioni yale ambayo nilitamani kuyasema. Mimi nitasema ya kwangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianzie nilipoishia kwenye Hotuba ya Waziri Mkuu kuhusiana na suala zima la hizi shule kongwe. Nadhani hapa sasa leo ndiyo hasa sehemu yenyewe. Niiombe sana Wizara ya TAMISEMI na kwa bahati nzuri wakati tunatembelea miradi tulikuwa na Mheshimiwa Dugange, anajua nilichoomba na naendelea kusisitiza kwenye taarifa hii hapa sasa hivi. Hebu tujitahidi, ni aibu kubwa shule kongwe ambayo hata Baba wa Taifa amesoma, inatia aibu. Naomba sana wasitegemee sisi Tabora eti mapato ya ndani yaweze kufanya karabati za shule zetu kongwe, haiwezekani kwa sababu hatuna fedha hiyo, kutokana na mapato yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shule hizo niongelee hata shule nyingine za msingi. Tuna Shule moja inaitwa Town School. Hii shule imeanzishwa mwaka 1940, ujenzi wa shule hii umetumia mawe. Hapa ninavyozungumza shule imechoka kweli kweli. Sasa nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mambo ya kuja Tabora waje watupe pole watoto wetu kule wameangukiwa na madarasa, jamani hatutaki. Kinga ni bora kuliko tiba. Nawaomba sana pamoja na shule nyingi kuwa kongwe na zina changamoto, lakini naomba hii Shule ya Town School waiangalie kwa jicho la peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombeni sana na niombe mbele ya Bunge hili tukufu mambo ya kuja kupeana pole, hapana. Tunaomba watusaidie hii shule ni ya toka mwaka 1940, ina changamoto, imechakaa sana na iko kati kati ya Kata yetu ya Gongoni. Kwa hiyo niombe sana Wizara iangalie hizi shule kongwe na hizi za msingi maana walikuwa wanahangaika na shule za sekondari na hizi za msingi nyingi zimechoka sana. Kwa hiyo tunaomba sana waweze kuzifanyia ukarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombee TARURA fedha. TARURA inahitaji kuongezewa bajeti. Mimi natoka Mkoa wa Tabora na hapa naomba nizungumzie hususan kwenye Jimbo ambalo natokea mimi la Tabora Mjini. Kwenye kata zetu kuna mitaa mbalimbali, kuna vijiji na kuna vitongoji. Barabara hazipitiki, leo nikikwambia hizo kata zetu za mjini barabara nyingi za ndani kwenye mitaa yetu ni barabara za vumbi. Hazina mitaro, mvua ni nyingi zikinyesha maji yanaingia kwenye nyumba za watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana wakati wanafikiria kununua magari ya ma-DC na ma-RC na watu wengine, tunaomba sana bajeti iongezwe kwenye TARURA. Wananchi wetu wanateseka, wanapata shida. Mvua zikinyesha maji yanaingia ndani. Sisi hatukatai ununuzi wa magari, wanunuliwe kwa sababu ni watendaji, lakini watapita wapi huko hawa ma-DC kama barabara ni mbovu. Lazima wawatengenezee na barabara kwanza ili yale magari watakapowanunulia waweze kupita kwenye sehemu salama. Wapunguze bajeti kidogo wazipeleke kwenye TARURA ili hawa watu waweze kufanya kazi vizuri jamani, wananchi wetu wanalalamika. Barabara za mitaani nyingi ni mbovu na especially sasa hivi mvua ndiyo zimekatika, wawape hizo fedha watu wa TARURA ili waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie juu ya hii miradi ya afya ambayo haikamiliki, ni aibu kubwa. Amezungumza Mheshimiwa Mbunge wa Itilima, Mheshimiwa Njalu. Amesema, hizi fedha wanazopeleka kwa maelekezo wanakosea. Maeneo mengine wananchi wameshatumia nguvu kubwa ya kujenga zahanati, vituo vya afya, wakiwapelekea fedha shilingi milioni 500 hii eti nendeni mkajenge kituo cha afya wanacha yale majengo waliyokuwa wameshayajenga, wanaenda kujenga majengo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepita huko Naibu Waziri wa TAMISEMI anajua, kuna majengo mengine ya afya yamekaa mpaka yameshachakaa hayajatumika kwa sababu ukiwauliza wameanza kujenga miradi mipya kwenye maeneo hayo badala ya kuwa wamepewa fedha ama TAMISEMI waulize kwenye maeneo wanayopeleka fedha, je, mnahitaji kujenga vituo vya afya maeneo gani na maeneo gani? Mnahitaji kujenga hospitali za wilaya zipi na zipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta hospitali ya wilaya tayari ilishajenga majengo saba, Serikali imepeleka fedha ya kujenga majengo mengine matatu. Yale saba yanaachwa, yanajengwa yale matatu ambayo zile fedha wamepeleka. Kwa nini zile fedha wasiwaambie kwamba wamalizie yale majengo ili watu waweze kupata kutumia hayo majengo. Fedha nyingi za Serikali zinazopelekwa, Mheshimiwa Rais anapeleka fedha nyingi lakini hazina thamani kwa wananchi kwa sababu hawatumii miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kidogo kwenye elimu wanajitahidi kwa sababu tunaona watoto wetu wanasoma madarasani lakini hawana madawati. Kuna mikoa ambayo unapita kuna baridi ya hatari. Sisi tumeenda Sumbawanga huko Rukwa, tumeenda Katavi kuna baridi kweli kweli. Wanajenga madarasa mawili mnatoa madawati 30, kila darasa madawati 15, 15. Darasa gani la Tanzania ambalo watoto wanakaa 45? Darasa moja watoto 100, watoto 70 watoto wote 40 unakuta wamekaa chini na baridi iliyoko katika mikoa hiyo mpaka unasikia huruma wewe mzazi tumbo linakucheza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwaombe wakati huu ambapo wako kwenye bajeti waweke bajeti wasaidie halmashauri zetu waweze kupata madawati. Pamoja na halmashauri zetu kujikongoja, lakini bado Serikali inatakiwa isaidie wananchi wetu, kule watoto wetu wa Kitanzania waweze kusoma wakiwa wamekaa kwenye madawati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie suala la hii 10%. Ni aibu kubwa, amezungumza Mheshimiwa Halima hapa na ndiyo ukweli ulioko huko chini. Hizi fedha hazijapotea hizi zipo. Kuna maeneo tumekwenda kuna kikundi cha familia; baba, kaka, mtoto wa baba mkubwa, mtoto wa mjomba, mtoto wa nani. Wamekaa sasa pale ehee, biashara gani ambayo mnafanya tunawauliza, wanaanza ooh, vikaenda vikarudi, vikafanyaje. Wamepewa zaidi ya shilingi milioni 30. Hiyo fedha inarudi na nini? Unawauliza wamebaki hawa, wawili. Sasa hawa wengine wako wapi? Wameingia mitini. Unamuuliza Afisa Maendeleo ya Jamii wakati unakuja kukikagua hiki kikundi ulijua kwamba hawa watu wakoje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi fedha kupitia Bunge lako Tukufu tunataka pamoja na kusimamisha mikopo ya 10%, hizi fedha kwanza zirudi. Zirudi fedha hizi za Watanzania walipakodi, wavuja jasho, halafu ndiyo tuanze mpango mzima wa kuhakikisha tunaanza kugawa tena hizi fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla hatujaanza kugawa fedha hizi huko kwenye halmashauri wapelekwe wataalamu wa fedha kwenye vikundi hivi ili waweze kusaidia wananchi wetu kujua miradi. Hawa maafisa maendeleo wa jamii mnaowapelekea hizi kazi si za kwao; na ndiyo maana maeneo mengi wamefeli kwa sababu hawana ushauri mzuri kwa vikundi wafanye biashara gani ili waweze kutoa marejesho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ajirini maafisa maendeleo ya jamii kwenye maeneo husika, na mnapoajiri msiajiri kwa upendeleo. Tumekwenda eneo moja jimbo lina kata 19, maafisa maendeleo wa jamii wako 43 wako kwenye jimbo moja. Katika mkoa huo kuna jimbo lina kata 27 lina maafisa maendeleo ya jamii wawili, kuna jimbo lingine kina kata 27 maafisa maendeleo wa jamii watatu. Sasa kata 27 zinafanywaje kazi maafisa maendeleo ya jamii 23? Hapo ndipo utakapoona huu ubabaifu wa hizi fedha unapoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha nyingine, watendaji wetu wasiokuwa waaminifu wa TAMISEMI, wanachukua fedha hizi kwa visingizio vya vikundi halafu wanazichukua wao wenyewe. Ndiyo maana tunasema hili Bunge tusikubali fedha hizi zipotee, hizi fedha lazima zirudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme, namshukuru Mheshimiwa Spika kwa kunipangia kwenye kamati ya LAAC, nitakuwa nasema kila siku hizi fedha mpaka zirudi ndipo zitoke fedha zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kwanza ya kuchangia katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na kuweza kusimama hapa na kuchangia katika Wizara hii. Nashukuru sana Wizara kwa kufanya maboresho makubwa katika bustani ya wanyamapori iliyopo pale Tabora Mjini. Wamefanya maboresho makubwa pale wameongeza wanyama wa aina mbalimbali, sasa hivi kuna simba, kuna chui, kuna pundamilia, kuna fisi kuna nyani na kuna ndege wa aina mbalimbali wakiwepo aina ya tausi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Tabora tunashukuru kwa sababu lile eneo lilikuwa ni pori, pori kabisa na ni eneo la Mjini karibia na Hospitali ya Kitete. Kwa hiyo, walivyoweka ile bustani kwa upande wetu sisi kwanza kabisa tumeshapata maeneo ya utalii. Sasa hivi Tabora imefunguka barabara za lami ni nyingi, hata sasa wanaokwenda Mwanza, wanaokwenda Kigoma, wanaokwenda Shinyanga wanaokwenda Kahama lazima wapitie Tabora ndiyo waweze kufika kwenye maeneo yao kutokana na barabara kuwa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niseme tu tunaendelea kuwakaribisha sana watu wote wa Tanzania wanaopita katika Mkoa wetu wa Tabora. Sasa hivi tuna bustani nzuri ambayo kuna wanyama wa kila aina tunatangaza utalii wetu wa Tanzania. Niwashukuru sana TAWA lakini naomba kuishauri Serikali endeleeni kuboresha eneo lile hasa kwenye masuala ya miundombinu ili kuweza kuongeza vivutio pia kuongeza watu ambao wanaweza wakaja pale kwa sababu watavutika na mambo mengi ambayo yatakuwa pale. Naamini bado lakini mtakuwa kwenye process hivyo naomba sana Serikali iweze kuongeza ili tuweze kuwa na vivutio vizuri katika Mkoa wetu wa Tabora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kidogo kuhusiana na maslahi ya watumishi. Ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri, Serikali mmeunda Jeshi Usu, Jeshi hili linafanya kazi kwenye taasisi mbalimbali za Wizara hii, lakini wote wanafanya kazi ya aina moja. Changamoto iliyopo na ambayo mimi niliiona na mpaka sasa naomba niiseme ni utofauti wa mishahara kwa watumishi hawa. Haiwezekani hawa mnawapa hiki, hawa mnawapa hiki wakati wote wanafanya kazi ya aina moja. Kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali ili kuondoa huu mkanganyiko, ili kuondoa kuombwa kuhama hama kwa hawa wafanyakazi, kwa sababu wengi wanatoka kwenye eneo ambalo halina mshahara mzuri wanataka waende kwenye taasisi ambazo zinalipwa vizuri kama TANAPA na NCAA. Kwa hiyo, hawa wengine wanaona kwa nini wakati sisi wote tunafanya kazi moja. Kwa hiyo, ninaomba sana na niiombe Serikali angalieni maslahi ya watumishi hawa, wawe na maslahi ya aina moja ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi hizi kazi ni ngumu, ngumu kwa wote. Wanaolinda mapori kazi ni ngumu na wanalinda hizi hifadhi zetu kazi ni ngumu. Kwa hiyo, wapeni maslahi yao ya aina moja ili wote waweze kufanya kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusiana na mapori ya akiba kwenye Kanda yetu ya Magharibi. Kanda ya Magharibi tunayo mapori ya Luganzo, Tongwe, Igombe, Ugalla, Inyonga na Wembera, haya mapori yameshapandishwa hadhi. Pamoja na kupandishwa hadhi hifadhi hizi zinasubiri kukamilika kwa zoezi la mapitio ya mipaka, zoezi hili lilianza lakini lilisimamishwa. Kwa hiyo, tunaomba sana zoezi hili liendelee ili mipaka hii waipitie, wakishaipitia pawekwe zile beacon ili wananchi wetu waweze kupata maeneo ya kufanya kazi kwa utaratibu mzuri ili kuondokana na kugombana baina ya wahifadhi pamoja na wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya ugomvi katika maeneo yao, hivyo tunashauri sana hii Kamati ambayo imeundwa, tunaomba sana iendelee na zoezi hili ili basi waweze kumaliza hii kazi na wananchi wetu waweze kuwa na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala lingine suala la Msomera. Kwanza kabisa mimi nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuamua kwa dhati kabisa kutaka kuiponya Hifadhi yetu ya Ngorongoro. Wananchi wa Ngorongoro walioamua kuondoka wenyewe kwa hiari wameshafika Msomera, lakini hawa wafugaji wameniomba niwaombee wanachangamoto kubwa ya maji pamoja na maeneo ya malisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba sana Serikali kupitia Wizara hii wawafanyie kila linalowezekana wafugaji hawa, kwa sababu wao wanachotegemea ni mifugo yao. Kazi nzuri iliyofanyika, nyumba nyingi zilizojengwa na wananchi ambao wameshahamia kule wanachoomba wapewe maji pamoja na maeneo ya malisho, mifugo ndiyo kitu wanachokitegemea katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wengine ambao wapo kule Ngorongoro wamekaa wanasubiri, Mheshimiwa Waziri kupitia Wizara yako tunaomba sana wale ambao tayari wanasubiri kwa hiari yao kuondoka kule kurudi huku fanyeni kila linalowezekana, malizeni huu mpango ili kuweza kuunga mkono juhudi za Mama. Kuweza kuhifadhi zaidi Mbuga yetu ya Ngorongoro na kuweza kuwa salama. Tulikuwa tukienda Ngorongoro unaanza kukutana na kondoo, ng’ombe, mbuzi lakini sasa hivi angalau hawajaisha lakini angalau kumepungua hata ukipita unaanza kuona, unajua kwamba kweli sasa hili ni eneo la uhifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba na mazungumzo pia yaendelee hata kwa wale ambao bado hawapo tayari muendelee kuwaomba siyo kuwalazimisha kama ambavyo mmefanya tangu mwanzo ili waendelee kuhama wenyewe kwa hiari, waweze kuondoka pale na waweze kwenda Msomera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Msomera sasa hivi shule zipo, tumeona kuna zahanati, tumeona kuna kila huduma za kijamii. Sasa changamoto iliyopo wapewe maji pia wapewe na maeneo ya malisho ili wasipate hamu tena ya kurudi Ngorongoro na kuanza tena kufukuzana kama ambavyo watu wanatarajia. Kwa sababu hili zoezi siyo watu wote walilipenda, hasa hata wenzetu majirani walilichukia na matokeo yake walianza kama kufanya hujuma lakini Mungu amebariki msimamo wa Rais wetu umekwenda vizuri na leo watu wengi wako Msomera kwa hiari yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalizungumza hili kwa sababu nilikwenda na nimejionea mwenyewe na tumpongeze sana Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya aliyeko sasa kwa kazi nzuri anayofanya ya kuhakikisha kwamba wananchi wanaendelea kuwa na utulivu na wanaendelea kupata mahitaji yao katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya muda naomba kushukuru kwa kunipa nafasi, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti hii ya 2023/2024. Kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia afya nami nimeweza kusimama na kuchangia bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nizungumze kwenye hizi barabara. Tumeona wenzetu wa Kusini sasa hivi wanasheherekea, wanashangilia wanasifia lakini yapo maeneo ambayo na sisi tumekuwa tukipiga kelele sana kuhusiana na barabara angalau za kuunganisha Mkoa na Mkoa ama Wilaya na Wilaya ambazo bado ni changamoto kubwa sana. Mimi ningeomba sana kwa Wizara ya Fedha tunayo barabara ambayo inatoka Mpanda inapita Kaliua kwenda Kahama, ningeomba sana na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi naye atusikie kwenye barabara hii, tumeshapigia kelele sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Tabora ni moja kati ya Mikoa ambayo kwanza ipo pembezoni lakini pili Mkoa wa Tabora ni moja kati ya Mikoa ambayo ina wakulima wengi, yaani sisi shughuli zetu za kutuingizia kipato ni kilimo. Sasa kama tunalima sana halafu tunakuwa hatuna barabara kwa ajili ya kusafirisha mazao yetu, hili jambo kwa kweli haliwezekani. Kwa hiyo, na sisi tuombe sana, tunaomba barabara inayotoka Mpanda kwenda Kaliua kufika Kahama ijengwe kwa kiwango cha lami ili iweze kurahisisha usafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo barabara ambayo inatoka Tabora Mjini inakwenda Bukene kupitia Mambali. Hii barabara nimeiongelea sana Mheshimiwa Naibu Waziri hapa aliniahidi mara kadhaa kwamba hii barabara itajengwa kwa kiwango cha lami. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie katika bajeti hii angalau hata kilomita chache ili zingine ziweze kuingia baadae, nakuomba sana tusaidie ili kuweza kusaidia wananchi wetu wanaotoka Tabora, badala ya kuzunguka kwenda mpaka Nzega ili waende wakatokee waende Kahama wapite hapa wapite Mambali-Bukene waingie Kahama na mwisho wa siku wanafika mpaka Mwanza. Kwa hiyo, itatusaidia pia kupunguza safari kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie kuhusiana na hili ongezeko la kwenye masuala ya Utalii. Bado tuna safari ndefu sana kama mpaka sasa tunazungumzia ongezeko la kutoka dola 1,310 tumefika 2,527 kwa nchi yetu ya Tanzania yenye vivutio vya kutosha, yenye vivutio vizuri, yenye mambo mengi ya ajabu, mpaka leo tunazungumzia 2,527, bado tuna safari ndefu. Tuna sema tuko kwenye asilimia 93, Tanzania sasa hivi tulitakiwa kuwa tunazungumzia asilimia180 mpaka 200 kwa jinsi tulivyokuwa na vivutio vizuri, tulivyokuwa na vivutio vya kutosha, tulivyokuwa na maajabu mengi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe Wizara ya Fedha huku mnapata fedha na nilishawahi kumwambia Mheshimiwa Waziri wa Fedha “ukitaka kula sharti uliwe”. Mheshimiwa Waziri wa Fedha anachukua fedha katika hizi taasisi lakini fedha hazirudi kule kwenda kutekeleza majukumu. TANAPA sasa hivi wanazo hifadhi 16, TAWA wana mapori ya akiba ya kutosha, TFS wana misitu chungu nzima, sikuambii na huko Ngorongoro lakini kote huko tunakusanya mapato, katika mapato yale lazima tufike mahali tukubali kutoa ili tuweze kutengeneza tupate zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwambia Mheshimiwa Waziri wa Fedha huku kuna hela, huku fedha ipo, lakini tuwekeze ilituweze kupata tija kwenye hili suala la utalii. Kama Mheshimiwa Rais aliamua kwa dhati ya moyo wake kutangaza utalii, kazi aliyoifanya ni kubwa sana, kama Wabunge tunaendelea kushauri Wizara iangalie kwa jicho la tatu kwenye hii sekta ya maliasili na utalii ili tuweze kuongeza mapato pia yaweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ya maliasili ina changamoto nyingi ikiwemo wafanyakazi wake kulalamikia maslahi yao, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha waangalie namna gani ya kuweza kuwasaidia watumishi hawa kuhusiana na maslahi yao, wanafanya kazi ngumu, wanafanya kazi hatarishi. Kwa kweli, mimi nimewahi kuhudumu kwenye Kamati hii ya Maliasili nimejionea mwenyewe, kuna maeneo unakwenda unasema hivi kuna Askari wako huku wanafanya kazi unaambiwa wapo wanafanya kazi. Sasa kwa nini tusiwaangalie na kuona ni namna gani tunavyoweza kuwasaidia ili kuweza kuongeza maslahi yao. Pia kazi hizi zinafanywa na wote ni za aina moja siyo tofauti lakini maslahi yao wanalipwa tofauti tofauti, sasa hii inavunja moyo wale wengine kufanya kazi kwa sababu wanaona kwa nini wengine wapate zaidi kuliko mimi wakati kazi tunayofanya ni ya aina moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Wizara ya Fedha liangalieni hili jambo, ondoeni matabaka ili kazi ziweze kufanyika kwa ufanisi. Kuna wakati mwingine mnasikia watu wanauawa, wanyama wanakufa, saa zingine watu wanakasirika wanaona ngoja na mimi nilale zangu bwana kwani nini? Lakini mkitengeneza mazingira mazuri kwa wafanyakazi wa sekta hii ya maliasili na utalii mimi naamini kabisa tutaongeza mapato kutoka hizo dola 2,527 tutafika mapa dola elfu tano na kitu, ushauri wangu kwa Wizara ninaomba sana wakichukua fedha wapeleke fedha ili kazi ziweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta hii ya utalii zipo taasisi za utafiti, hizi taasisi haziguswi kabisa, yaani hata ukifika bajeti yao yenyewe pia inakuwa haieleweki. Kwa hiyo mimi niombe sana kwenye Wizara ya Fedha angalieni hizi taasisi za utafiti ili ziweze kufanya kazi zao vizuri na waweze kuongeza tija katika suala zima la utalii katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapokuwa mwanasiasa ni lazima uwe unaangalia mambo yote yanayoendelea, unasikiliza unajua kwamba wapi nini kinafanyika. Juzi katika harakati zangu nilimskia Mheshimiwa Katibu Mkuu wa CCM Mheshimiwa Chongolo akiwa Kondoa, migogoro inapunguza sana kasi ya uchumi katika nchi yetu, kama hatukuwa makini huu uchumi tunaouimba utaishia kwa watu ambao huku Mjini tu, lakini kwenye maeneo yenye migogoro tutausikia kwenye bomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Katibu Mkuu wa CCM Mheshimiwa Chongolo alikuwa kule kwenye pori la Mkungunero. Pale Mawaziri Nane wameshakwenda na pori lile wakasema kwamba tayari wameshalishughulikia lakini mpaka hivi tunavyozungumza wananchi wamekwenda kulalamika mbele ya Mheshimiwa Katibu Mkuu wa CCM. Nazungumza hivyo kwa sababu Tabora tuna mgogoro uliopo Kaliua na mgogoro huu hauna sababu hata kidogo, Mawaziri Nane wamekwenda katika Jimbo la Kaliua, Kata ya Ukumbikakoko na Usinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mawaziri hawa walisema hawa wananchi Mheshimiwa Rais ameruhusu waendelee kukaa hapa hapa na ikiwezekana waongezewe na maeneo mengine pale, kwa sababu Serikali haina mpango wa kuyachukua. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kujali wananchi hawa, lakini cha ajabu Mawaziri Nane wameondoka kinachoendelea huko ni mgogoro ambao mtakuja kusikia mauaji ambayo hayana hata sababu zozote za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia uchumi lazima uwaguse Watanzania wote bila kujali watu wanaishi wapi. Sasa hawa wanaoishi na migogoro, ambao hawajui kesho yao itakuwaje leo Mheshimiwa Rais ameruhusu wananchi hawa waendelee kubaki lakini anakuja mwingine ndani ya Serikali hiyohiyo anapinga maoni ya Mawaziri Nane walivyokuja na kauli ya Mheshimiwa Rais. Sasa hivi tuseme hii Serikali iko tofauti ama shida ni nini?

Mheshimiwa Mwenyeekiti, nimeona niliseme hili ili mjue kwamba tunapozungumzia bajeti humu, tunapowasemea Watanzania, tunapomshukuru Mama kwa kuleta bajeti ya Watanzania lakini ajue kuna Watanzania ambao hawanufaiki na haya tunayoyazungumza kwa sababu ya migogoro waliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe sana kama inawezekana watenge fedha ziweze kusaidia hii migogoro iweze kupungua. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru naitwa Hawa Mwaifunga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na nimeweza kusimama tena katika Bunge hili na mimi niweze kuchangia hoja ya Wizara hii ya Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Wabunge wenzangu wametangulia kuzungumza nami naomba niseme mambo yafuatavyo; naomba na mimi nijielekeza kwanza kwenye hii Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tume hii kwangu mimi ndiyo niliona muarubaini wa kupunguza migogoro ya ardhi katika nchi hii. Lakini tume hii ina sheria nzuri, tume hii imejiandaa vizuri katika kutekeleza majukumu yake, tume hii ina kiongozi mzuri ambaye ni Profesa na maandiko yao ni mazuri kabisa ukiyaona kwenye makaratasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini changamoto kubwa iliyopo ni ukosefu wa fedha. Haiwezekani nchi hii ikatulia, nchi hii ikapata amani ya migogoro kama tume hii haijaingia kazini kwenda kupanga matumizi ya ardhi kwenye vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kwenye Ilani yenu ya Chama cha Mapinduzi mmesema angalau kila mwaka vijiji 750 viende vikapimwe. Leo mnatoa fedha ya vijiji 100 vikapimwe, hivi vijiji 3,000 ambavyo mnasema ndani ya miaka mitano viwe vimeshapimwa vitafika lini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yangu mnapotoa fedha huwa mnaangalia kwanza Ilani halafu ndiyo mnakwenda kutoa fedha. Sasa kwa nini hii tume imewekwa nyuma wakati imo ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi? (Makofi)

Kwa hiyo, niombe sana kama ambavyo wenzangu wamesisitiza, tunaomba sana Kamati ya Bajeti, Serikali, Waziri wa Fedha wakae, waangalie namna bora ya kuweza kumsaidia Mheshimiwa Waziri Mama Mabula aweze kufanya kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu inafika mahali Wabunge tunashindwa kuzungumza vizuri kwa sababu tutasema nini wakati huyu mama bado hajapewa fedha? (Makofi)

MBUNGE FULANI: Ndiyo.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, hebu mpeni fedha, halafu ashindwe kufanya kazi ili tusimame hapa tuseme. Kwa sababu sasa hivi hata tukisema tutakuwa tunamuonea na huku ndiyo kwenye eneo mahususi ambalo anaweza kufanya kazi vizuri na kwenda kupunguza migogoro ya ardhi iliyokuwepo. Wanapambana sana kupunguza hii migogoro. Leo kuna Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya, kuna Mabaraza ya Ardhi ya Kata, kama hii tume ikiwezeshwa hata haya mabaraza yatakuwa hayana kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na huku kwenye mabaraza kesi nyingi sana unazokutana nazo za migogoro ya ardhi wengi wanaoteseka ni wakinamama tena wajane. Ifike mahali tuwaonee huruma hawa wanawake, kwanza wamefiwa na wanaume zao, lakini pili bado wanapambana na migogoro hii ya ardhi. Kila siku kwenda na kurudi kwenye haya Mabaraza ya Ardhi kwa kweli ni mtihani mkubwa. (Makofi)
Kwa hiyo, niombe sana na mimi kama Mjumbe wa Kamati hii na tulishaomba na ninarudia tena, bila fedha hizi kuwapa hawa tume, hakuna kitu kitakachoweza kufanyika kupunguza migogoro hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe shilingi bilioni 10 walizoomba siyo nyingi, ni hela kidogo sana kama alivyozungumza ndugu yangu jana hapa, ni hela kidogo sana ambayo Serikali haishindwi kutoa hii fedha ili hawa Mawaziri na watendaji wao waende wakafanye kazi. Tunahitaji angalau vijiji 750 angalau viweze kupimwa jamani tupunguze hii migogoro kupangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tumekwenda Singida Vijijini, Kijiji cha Ntondo na Kijiji cha Nkwae tumejionea wananchi wale wakiwa na furaha baada ya kupangiwa maeneo yao. Kwa hiyo, sasa hivi hakuna mtu anayeweza kwenda kuvamia pale Nkwae na Ntondo. Kwa sababu wale wananchi wameshatengenezewa mazingira mazuri na kila unayemuuliza anakwambia hapa ni hiki, hapa ni hiki, hapa ni hiki, hapa ni hiki. Nani atakuja kuvamia? Ili tupunguze hata mauaji ya wakulima na wafugaji? Tupange matumizi bora ya ardhi, hakuna mtu atakayeweza kuja kuvamia kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Mawaziri Nane; mimi nipo kwenye Kamati ya Ardhi na tuliomba hapa na kuna mwenzetu mmoja aliomba mwongozo. Kamati hii ilikuwa haijawahi kutoa taarifa, tulivyoomba walikuja wakatupa taarifa kidogo. Kwa taarifa ile ambayo wametupa, ninachokiona badala ya kwenda kutatua changamoto za migogoro ya ardhi tumekwenda kufukua moto ambao sijui huko mbele hali itakwenda kuwa namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mawaziri nane wanapokwenda kwenye Majimbo ya watu na kwenye Mikoa ya watu waonane na wananchi na siyo kuishia kwenye Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, waende kwa wananchi. Wanakwenda kwa wananchi wakikuta sehemu imetulia, lakini wakikuta sehemu moto unafuka, hawaendi wanaishia kwenye Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya. Inawezekana kabisa hii Kamati ya Mawaziri Nane ikawa ni mwiba mchungu kwa wananchi kuliko ilivyo kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa dada yangu Angeline Mabula mkienda kule, nendeni mkawaone wananchi waambieni ambacho mnakwenda kukifanya. Zile kamati zetu ndogo mnazoziacha kule chini ndiyo mwiba mchungu kwa wananchi na kila siku nawaambia mtakuja kukuta mambo ambayo hamkuyategemea huko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la kurasimisha. Hili jambo sisi labla pengine kama Wajumbe wa Kamati tunaweza tukawa tumelielewa na baadhi ya Wabunge. Lakini wananchi huko hawalielewi hasa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam. Naomba sana watakapokuja ku-windup hapa waeleze hili zoezi la kurasimisha lina maana gani na nini kifanyike ili wananchi wale waweze kulielewa, vingingeno mtakuwa mnatangwa maji kwenye kinu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo naomba. Wizara hii inahitaji wafanyakazi. Waongezewe wafanyakazi ili kazi ziweze kufanyika kwa ufanisi mkubwa kuliko ilivyo hivi sasa, wafanyakazi ni wachache, kazi ni nyingi, wanahitaji kufanya mbambo mengi kuliko uwezo walionao wa wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la mwisho naomba nijikite kwenye Mkoa wangu wa Tabora, hususan kwenye Manispaa ya Tabora Mjini ambako mimi ni Diwani kwenye Manispaa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Tabora Mjini waliamua kutoka mjini na wakaenda kwenye eneo la nje ya mji ambalo linaitwa Ndevelwa. Eneo lile limepimwa viwanja na wananchi wamepewa hati. Lakini watu wa TARURA mpaka sasa bado hawajapeleka miundombinu ya barabara ili wananchi wale waweze kuonyeshwa maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Wizara ya Ardhi mshirikiane na Wizara ya TAMISEMI, watu wa TARURA wapeleke barabara ili wananchi waweze kuoneshwa maeneo yao. Haiwezekani mtu ana hati mkononi halafu eneo lake halijui, eneo langu ni lipi. Kwa hiyo, naomba sana watu wa Wizara hakikisheni wananchi hawa wanajua ili watu waweze kulipia zile hati, tuweze kupata fedha kwa ajili ya kutatua migogoro iliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo naliomba, naomba sana na naomba nisisitize sana kwa Wizara, fanyeni ukarabati kwenye nyumba za National Housing, yamekuwa kama magofu, tumechoka kuona hali hizi ikiwemo kwenye Manispaa yangu ya Tabora, yaani zile nyumba zimezeeka pamoja na kwamba Tabora ni mji mkongwe lakini tunaomba mtusaidie zile nyumba zenu pale ziko nyingi lakini zote hazifai zimechakaa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante. Ahsante kwa mchango. Ahsante, unga mkono hoja.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Unga mkono hoja.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi/Kicheko)