Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Ally Mohamed Keissy (7 total)

MHE. ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Kituo cha Polisi cha Marine Kipili, hakina usafiri wa nchi kavu:-
(a) Je, ni lini Serikali itakisaidia kitu hicho usafiri wa nchi kavu angalau hata kukipatia pikipiki?
(b) Je, ni lini Serikali itaongeza mgao wa petroli?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally KeissyMohamed, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi Karibuni Serikali imegawa vyombo vya usafiri takribani kwa Wilaya zote, ikiwemo Wilaya ya Nkasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Kipili kimo ndani ya Wilaya ya Nkasi kikihudumiwa na gari Namba PT 3836 ambayo ni jipya lililotolewa hivi karibuni. Hata hivyo, utaratibu utafanyika ili wapewe pikipiki iweze kusaidia kupunguza tatizo la usafiri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaongeza mgawo wa mafuta kulingana na hali ya uchumi itakavyoimarika.
MHE. ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Serikali imekwishatumia zaidi ya shilingi milioni 800 kwa ajili ya Mradi wa Skimu ya Lwafi, lakini mradi huu haujawanufaisha kabisa wakulima zaidi ya 4000 kwa sababu haujakamilika:-
Je, ni lini Serikali itapeleka fedha ili kukamilisha mradi huo ili uwe wa msaada kwa wakulima wa mpunga zaidi ya elfu nne?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Keissy, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi wa Tarafa ya Kilando kuhusu uendelezaji wa kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Mto Lwafi, ilianza kuboresha miundombinu ya umwagiliaji katika skimu husika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Mnamo mwaka 2012, banio lilijengwa na mfereji mkuu wa urefu wa kilomita 1.6 ulichimbwa na kusakafiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia mkopo kutoka Serikali ya Japan, Serikali inategemea kupeleka fedha katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mwezi huu Juni, 2016. Fedha hizo zitatumika kuchimba sehemu ya mfereji mkuu wenye urefu wa kilomita 16 na kusakafia na kujenga maumbo ya maji ndani ya mfereji huo. Hatua hiyo itawezesha wakulima wa mpunga katika skimu hiyo kunufaika.
MHE.ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Vituo vya Polisi vya Kabwe na Kirando vimechakaa sana na hata polisi hawana nyumba za kuishi:-
Je, ni lini Serikali itajenga au kukarabati vituo hivyo na kuwajengea polisi nyumba za kuishi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Keissy, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango wa kukarabati, kujenga makazi na vituo vya Polisi nchi nzima ikiwemo Kabwe na Kirando kwa awamu. Kwa upande wa makazi ya Askari Polisi awamu ya kwanza ya ujenzi itajumuisa nyumba 4,136. Kwa vituo ambavyo ni chakavu Serikali itaendelea kuvifanyia ukarabati kulingana na uwezo wa fedha kadri utakavyoruhusu.
MHE. ALLY M. KEISSY aliuliza:-
Mheshimiwa Rais alipokuwa Wizara wa Ujenzi wakati wa Awamu ya Nne aliahidi kwamba baada ya barabara ya Sumbawanga - Mpanda kukamilika kwa lami majengo yaliyopo katika kijiji cha Paramawe, Wilayani Nkasi yatatumika kwa ujenzi wa VETA, hasa ikizingatiwa kuwa Wilaya ya Nkasi haina chuo hicho.
(a) Je, Serikali iko tayari kutumia majengo hayo kwa ajili ya chuo cha VETA?
(b) Je, Serikali, iko tayari kwenda kuyaona majengo hayo mara barabara itakapokamilika?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Keissy, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, (a) napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ipo tayari kutumia majengo yaliyopo katika kijiji cha Paramawe, Wilayani Nkasi ambayo ni kambi ya ujenzi wa barabara ya lami ya Sumbawanga - Mpanda kwa ajili ya Chuo cha Ufundi Stadi chini ya Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi (VETA) ili kuweza kutoa mafunzo ya ufundi stadi baada ya kukamilika kwa ujenzi wa barabara hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, (b), Serikali pia ipo tayari kutuma wataalam kutoka wa VETA kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kwenda kuyaona majengo hayo mara barabara hiyo itakapokamilika kwa lengo la kufanya tathimini na kujiridhisha juu ya ubora wake kwa ajili ya kutoa mafunzo ya ufundi stadi. Hata hivyo, majengo hayo tatatumika kutolea mafunzo ya ufundi stadi baada ya kukamilika kwa taratibu za kupata idhini kutoka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambao ni wamiliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa ushauri kwa wananchi wa Wilaya ya Nkasi waendelee kutumia Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Chala, kuwapatia ujuzi vijana wakati juhudi za Serikali, za kuwatafutia chuo cha ufundi zikiendelea.
MHE. ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Serikali imekwishatumia zaidi ya shilingi milioni 800 kwa ajili ya Mradi wa Skimu ya Lwafi, lakini mradi huo haujawanufaisha kabisa wakulima zaidi ya 4,000 kwa sababu haujakamilika:-
Je, ni lini Serikali itapeleka fedha ili kukamilisha mradi huo na kuwa msaada kwa wakulima wa mpunga zaidi ya 4,000?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Keissy, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi wa Tarafa ya Kirando inaendeleza kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Mto Lwafi. Hadi sasa eneo la Awamu ya Kwanza la hekta 300 linaweza kumwagiliwa kati ya hekta 2,500 zilizokuwa zimetengwa. Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji inaendelea kutafuta fedha ili kuhakikisha eneo lote la hekta 2,500 zilizopimwa na kusanifiwa mwaka wa 2012/2013 zimejengewa miundombinu ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha eneo lote la hekta 2,500 zilizopimwa na kusanifiwa zinajengwa miundombinu, Serikali ilifanya marudio ya usanifu uliokamilika mwezi Septemba, 2016. Usanifu huo wa mapitio ulifanyika kulingana na hali ya sasa katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza awamu ya pili ya utekelezaji wa skimu hiyo kwa kupata fedha za mkopo kutoka Serikali ya Japan, ambapo jumla ya shilingi milioni 580 zimepelekwa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji. Kazi zitakazofanyika ni pamoja na kuchimba mifereji ya kati yenye urefu wa mita 16,000, kujenga kivushamaji chenye urefu wa mita 200 kwa kuvuka mto Lwafi na kujenga vigawa maji 28 katika mifereji ya kati.
Mheshimiwa Spika, kazi hizo zitakapokamilika, eneo litakalomwagiliwa litafika hekta 800 kati ya hekta 2,500 zilizosanifiwa. Serikali itaendelea kutafuta fedha kupitia vyanzo mbalimbali ili kuhakikisha kwamba eneo lote la hekta 2,500 linajengewa miundombinu ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inaendelea na taratibu za kuwapata Wakandarasi wa Ujenzi wa miundombinu iliyopangwa; na makabrasha ya zabuni kwa ajili ya kuwapata Wakandarasi hao, yamekamilika.
MHE. ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Kutokana na ahadi ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa alipokuwa Waziri wa Ujenzi na sasa ahadi aliyoitoa akiwa Rais wakati wa kampeni zake za uchaguzi kwamba barabara ya Kirando – Kazovu –Korongwe yenye urefu wa kilometa 35.6 ingejengwa kwa sababu Halmashauri haina uwezo wa kuijenga.
Je, ni lini Serikali itaanza kuijenga barabara hiyo ili iwasaidie wananchi wa vijiji vya Katete, Chongo, Isaba na Kazovu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Keissy Mohamed, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Kirando -Kazovu - Korongwe (kilometa 35.6) inahudumiwa na Halmashauri ya Wiaya ya Nkasi na haijawahi kuhudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).
Hata hivyo, Serikali kupitia TANROADS Mkoa wa Rukwa ilifanya tathmini ya awali ya barabara hii ili kuweza kujua hatua za kuchukua kwa nia ya kuifungua. Katika tathmini hiyo zilionekana changamoto mbalimbali ambazo ni pamoja na barabara kupita kwenye milima, mabonde, mbunga, mapori na milima yenye miamba. Barabara hii inahitaji kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili iweze kujengwa kikamilifu. Kwa sasa Serikali inatafuta fedha ili kukamilisha kazi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuiwezesha barabara hii kupitika, katika mwaka wa fedha katika mwaka wa fedha 2016/2017, kiasi cha shilingi 705,000,000 zimetengwa zikiwa ni fedha za maendeleo kutoka Umoja wa Ulaya (EU) kwa ajili ya kuanza kujenga kilometa 15 za mwanzo za barabara hii kwa kiwango cha changarawe. Zabuni kwa ajili ya matengenezo ilitangazwa tarehe 15/02/2017 na kufunguliwa tarehe 07/03/2017 ambapo mkataba wa kazi ya matengenezo unatarajiwa kusainiwa tarehe 18/05/2017 yaani kesho.
MHE.ALLY K. MOHAMED aliuliza:-
Katika miaka ya 1960 kulikuwa na Kingo katika Mto Lukuga huko DRC- Congo; kingo hizo zilisaidia sana kuzuia kupungua maji katika Ziwa Tanganyika:-
Je, nchi za Burundi, Zambia, DRC-Congo na Tanzania zimefikia wapi katika mpango wa kuweka kingo katika Mto Lukuga ili Ziwa Tanganyika lisiathirike sana kwa kupungua maji na kutishia uhai wa viumbe katika ziwa hilo?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Keissy Mohamed, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana kwa kufuatilia hili jambo kwa muda mrefu. Tatizo la kushuka kwa kina cha maji katika Ziwa Tanganyika ambalo kwa kiasi kikubwa limesababishwa na kubomoka kwa banio la maji kwenye Mto Lukuga (DRC) linafuatiliwa kwa karibu na Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mto Lukuga ndio mto pekee unaotoa maji kwenye Ziwa Tanganyika upande wa DRC kupeleka Mto Congo na hatimaye kwenye bahari ya Atlantiki. Aidha, Serikali za DRC na Tanzania kwa pamoja zinamiliki asilimia 86 ya Ziwa lote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kushuka huko kwa kina cha maji ya Ziwa kumeathiri shughuli za kiuchumi na kijamii ikiwemo, meli kubwa kushindwa kutia nanga ili kupakia na kupakua mizigo na abiria kwenye bandari za ziwa hilo. Bandari hizo ni pamoja na bandari za Kigoma na Kasanga kwa upande wa Tanzania, Bujumbura Burundi, Kalemia, Uvira na Moba kwa upande wa Congo. Aidha kwa upande wa Tanzania chanzo cha maji kwa Mji wa Kigoma Ujiji pia kinaathirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na mwezi Machi, 2014 Wakuu wa Nchi za Tanzania na DRC waliagiza Mawaziri wa nchi hizi mbili wanaoshughulikia masuala ya maji wakutane ili kujadili namna ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa banio la Mto Lukuga lililobomoka. Mawaziri hao walikutana mwezi Aprili, 2014 na Agosti, 2014.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya vikao hivyo Serikali hizi mbili zilitiliana Hati ya Makubaliano tarehe 7 Mei, 2015 ambapo zaidi ya dola za Kimarekani milioni sitini na tano zinahitajika kujenga banio lililobomoka. Pia nchi za Burundi na Zambia ambazo ni wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika zimeshirikishwa katika suala hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 7 – 9 Machi, 2016 kuliandaliwa Mkutano wa Wadau wa Maendeleo uliofanyika Nchini DRC na kuhudhuriwa na wawakilishi wa Benki ya Dunia ambapo walituma wataalam ili kufanya tathmini ya awali kuhusu tatizo la kupungua kwa kina cha maji. Aidha, jitihada nyingine za kutafuta fedha zinaendelea kwa kuwashirikisha wadau wengine wa maendeleo.