Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Jumaa Hamidu Aweso (423 total)

MHE. MAHMOUD H. MGIMWA: Mheshimiwa Spika, pamoja na maelezo ya Serikali, nina swali moja na ombi moja.
Ombi, namuomba Mheshimiwa Naibu Waziri mara baada ya Bunge hili aje pale kwenye Kijiji cha Nundwe atembelee mradi huu aweze kujionea hali halisi na mahitaji ya mradi huu ambao unatarajia kuajiri vijana wasiopungua takribani 5,000.
Mheshimiwa Spika, swali langu, mradi huu ni miongoni mwa miradi ya FP I ambao ulikuwa na thamani ya milioni 660. Mheshimiwa Waziri Mkuu Mstaafu alipokuja kufungua mradi huu, tayari shilingi milioni 101 zilikuwa zimeshatumika lakini ilionekana kulikuwa kuna mahitaji ya shilingi milioni 295 ili mradi uweze ku-take off.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu aliahidi kwamba baada ya miezi mitatu shilingi milioni 295 zingekuwa zimefika, maana zingekuwa zimefika Juni, 2015, lakini mpaka leo hizi hela hazijafika. Sasa nataka Mheshimiwa Naibu Waziri aniambie, lini watatuletea hizi hela, shilingi milioni 295, ili vijana waweze kupata ajira?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, moja, kuhusu ombi la mimi kwenda katika Kijiji cha Nundwe, nataka nimhakikishie, kwa kuwa anayelala na mgonjwa ndio anayejua mihemo ya mgonjwa, nipo tayari kwenda kuukagua mradi ule ili usikwame, ili uweze kuleta uwezeshaji wa kiuchumi na chakula cha kutosha kwa kijiji kile. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu swali la pili; lengo la Serikali ni kukamilisha miradi yote ili iwe endelevu katika suala zima la utekelezaji. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutatafuta fedha katika vyombo mbalimbali ili kuhakikisha fedha zile zinapatikana ili mradi usikwame uende kutekelezwa mara moja. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa vile mradi huu ni wa siku nyingi unaenda miaka saba sasa na Serikali imetoa commitment kwamba mwezi Desemba, 2017 itaanza utekelezaji. Sasa kwa sababu ni wa muda mrefu mwezi Desemba isipoanza utekelezaji nini kifanyike?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Waziri wa Maji tuliwasiliana naye kuhusiana na maji Kata za Igohole, Nyololo na Mninga na niliagizwa kwamba tupeleke andiko linaloonyesha gharama za utekelezaji wa maji katika vijiji hivi nilivyotaja na andiko lile nimeshapeleka na gharama zote, liko kwa Katibu Mkuu. Sasa lini utekelezaji wa maji katika Vijiji vya Igohole na Nyololo utafanyika kwa sababu hawana maji kabisa na hivi ninavyoongea hawana maji. Ni lini Serikali itatekeleza? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji na kwa kuwa maji ni uhai na pasipo maji hakuna uhai, labda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama ilivyoahidiwa kwamba mwezi Desemba mradi ule unatekelezwa na mimi kama Mheshimiwa Waziri nitasimamia na kusukuma kuhakikisha kwamba mradi ule unatekelezwa ili wananchi wa eneo lile waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili kuhusu andiko na umuhimu wa suala la maji labda nimwombe sana Mheshimiwa Mbunge kama anavyowapigania wananchi wake baada ya kikao cha Bunge tukutane na mimi nipate nafasi ya kupitia andiko lile tuangalie namna ya kuweza kuwasaidia wananchi wa Igohole na Nyololo. Ahsante sana.
MHE. SONIA J. MAGOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa tatizo la wananchi wa Mufindi Kusini linafanana kabisa na tatizo linalowakumba wananchi wa Handeni Mkoani Tanga. Je, Serikali ina mpango gani kuondoa au kupunguza adha hii ya maji inayowakuta wananchi wa Handeni? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwanza katika bajeti ya mwaka 2017/2018 kumetengwa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa maji. Pia wananchi wa Handeni wapo katika mradi ule wa HTM. Sisi kama Wizara tutasimamia mradi huu wa maji ili uweze kutekelezwa wananchi waweze kupata maji. Ahsante sana.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Matatizo yaliyopo katika Jimbo la Mufindi Kusini yanafanana kabisa na matatizo yaliyoko katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki. Tuna mradi wa maji katika vijiji vitano una miaka zaidi ya tisa. Serikali imejitahidi kujenga miundominu yote ya kuhifadhi na kusambaza maji kwa kutegemea chanzo cha Mto Ruvu katika mradi wa Chalinze III lakini mpaka leo maji hayatoki. Nataka kujua ni lini Vijiji hivi vitano vya Maseyu, Kinonko, Kidugalo, Ngerengere, Sinyaulime pamoja na kambi mbili zetu za Jeshi za Kizuka na Sangasanga vitapata maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Mheshimiwa Mgumba kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake. Kwa kuwa suala la maji ni maisha ya watu, labda nimwombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge na mimi nipate nafasi ya kuweza kufika Morogoro Kusini Mashariki ili tuweze kuzungumza na wananchi na kuangalia namna gani tunaweza kuchukua hatua za haraka ili kuweza kuwasaidia wananchi wale kuondokana na adha ya maji. Ahsante sana.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na kutaja vizuri vijiji hivi, nina swali la nyongeza. Mwaka jana bajeti yetu ilikuwa shilingi bilioni 2.4 ikarudi na sasa hivi Mheshimiwa Waziri amesema tumetengewa shilingi bilioni, tatizo lililoko pale ni kwamba wakandarasi wanaojenga miradi hiyo baadhi yao hawako site ndiyo maana bajeti mwaka jana imerudi na kadri inavyoendelea hivi bajeti ya mwaka huu kuna wasiwasi wa kurudi. Je, atanisaidiaje kusukuma sasa bajeti hii iishe kwa kuwa wakandarasi wengi hawako site?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mradi wa Haydom mpaka sasa una tatizo la kwisha pamoja miradi hii ambayo ameitaja mwenyewe ya Arri-Harsha, Barshai, Quantananat na mradi wa Mongahay kuja Tumati. Je, atakuja lini kule na kuwaahidi wananchi wangu ili aweze kuona jinsi ambavyo wakandarasi wanawadanganya kutomaliza miradi na pesa za maendeleo kurudi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ya pekee anavyowapigania wananchi wake wa Mbulu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ieleweke kabisa nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji, si maji tu bali ni maji safi na yenye kutosheleza. Hata hivyo, imeonekana baadhi ya wakandarasi wamekuwa wakikwamisha jitihada za Serikali. Labda niziagize tu Halmashauri kwa wakandarasi ambao wanakwamisha miradi ya Halmashauri waondolewe mara moja kwa mujibu wa mikataba yao waliyoingia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niwaombe sana Wakurugenzi wasiwape kazi wakandarasi kishemejishemeji au kiujombaujomba, wananchi wanapata tabu wakati Serikali inatoa fedha. Kikubwa naomba wale wakandarasi wanaokwamisha miradi waondolewe mara moja wapatikane wapya ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, kuhusu suala la mimi kufanya ziara katika Jimbo la Mbulu, nipo tayari baada ya Bunge tunaweza tukaongozana pamoja kwenda kuzungumza na wananchi wa Mbulu. Ahsante sana.
MHE. SEIF K. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kufahamu, je, Serikali ina mpango gani ya kusambaza huduma hii nchi nzima hasa katika Wilaya ya Igunga na Mkoa wa Tabora na ukifuatilia kwamba katika Wilaya ya Igunga na Mkoa wa Tabora hivi karibuni tutaweza kupata maji ya Ziwa Victoria?
Mheshimiwa, la pili, nilikuwa nataka kujua juu ya Wizara hii ya Maji, inatoa tamko gani kwa baadhi ya Mamlaka za Maji nchini ambazo zinatoa bili kubwa kwa watumiaji wa maji kuwabambikiza bili kubwa watumiaji wa maji kuliko matumizi halisi ya wananchi wanaotumia kwenye maji? Nataka kujua tamko la Serikali juu ya ubambikizaji wa gharama za maji, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyopigania wananchi wake. Lakini kikubwa napenda kujibu maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni kuhusu suala zima la usambazaji mkakati wetu kama Serikali. Safari ni hatua na hatua tumeshaianza ya kutekeleza mamlaka saba na kwa kuwa safari moja huanzisha nyingine sisi kama Serikali kwa kupata nafasi ya kuweza kutekeleza mamlaka saba tunaziagiza mamlaka zote zenye uwezo wa kujitosheleza kigharama kutenga bajeti kuhakikisha kwamba wanatengeneza mifumo hii ili kuweza kuyafikia maeneo ya mbali katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, katika baadhi ya mamlaka kuwabambikia wananchi ama wateja gharama ambazo si halisia haipendezi, wala haifurahishi, kuona baadhi ya mamlaka zinawabambikia bei wananchi. Mimi nataka niziagize mamlaka zote nchini kwamba watoe bei halisia ambazo zimeidhinishwa na EWURA. Kama kuna mtu au mamlaka itakayokaidi hata kama ana mapembe marefu kiwango gani tutayakata ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata huduma bila usumbufu wowote.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyoko katika Jimbo la Manonga linafanana kabisa na changamoto iliyoko katika mkoa wangu wa Ruvuma. Katika mkoa wa Ruvuma kuna changamoto ambayo itaenda sambamba na tatizo la kubadili mita za maji kutokana na mfumo wa kupata maji kwa maana ya mita ibadilike kuwa wananchi wapate maji kwa mfumo wa unit. Sambamba na hilo, iko miradi ambayo nilikuwa nikisema hapa mara nyingi katika mkoa wangu wa Ruvuma ambayo kimsingi inaonekana kwamba imekamilika laikini haitoi maji, na miradi hiyo inataokana na World Bank.
Mheshimiwa Mwenyekiti, World Bank wamefanya hiyo kazi na miradi inaonekana kwamba sasa tayari inatoa maji, lakini katika miradi hiyo kuna mradi wa maji wa Mkako (Mbinga), Ruhuwiko (Songea Mjini), Matemanga na Ndembo (Tunduru), Litola (Namtumbo)...
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango gani ya kuhakikisha miradi hii inafanyiwa marekebisho ili iweze kutoa maji na wananchi waweze kufaidika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema kwamba miradi imekamilika lakini maji haitoi kwa wananchi. Lengo la Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji na fedha zimetolewa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ile. Lakini cha kushangaza miradi imekamilika haitoi maji. Labda nimuombe Mheshimiwa Jacqueline kwamba baada ya Bunge tuongozane pamoja tukaone sababu gani zinazosababisha mradi ukamilike lakini hazitoi maji? Kama kuna mtu ambaye anasababisha au kukwamisha ili maji isitoe tutalala naye mbele ili wananchi wetu waweze kupata maji.
MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Wakati tunasubiri utaratibu wa kupata maji hayo ya uhakika ya hiyo progamu ya pili ya maji hayo kutoka Ziwa Victoria, je kwa sasa Serikali ina utaratibu gani wa haraka wa kusaidia kutatua maji katika Jimbo la Igalula?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari baada ya Bunge hili kwisha, kuambatana na mimi kwenda katika Jimbo la Igalula kuona shida kubwa ya maji ya wananchi wa Jimbo la Igalula? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Musa Ntimizi kaka yangu, Mbunge kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake wa Igalula.
Mheshimiwa Spika, mkakati wetu, pamoja na ujenzi wa bomba la kutoka Ziwa Victoria mpaka Uyui na maeneo mengine, lakini moja ya mkakati wetu kama Wizara, Serikali na Mheshimiwa Rais nia yake ya kuwatua akinamama ndoo kichwani, tumetenga bajeti katika kila Halmashauri na Halmashauri ya Igalula imetengewa fedha katika bajeti hii ya 2017/2018. Kwa hiyo, mkakati wetu ni kusimamia kwamba wanatengenezewa visima vya haraka ili wananchi wetu wa Igalula waweze kupata maji.
Mheshimiwa Spika, kukamilika kwa mradi huu wa Ziwa Victoria kutatupa fursa sisi kama Wizara kuangalia namna gani wananchi wa Igalula wanaweza kunufaika kupitia hili bomba kuu. Hii ni kwa sababu Waswahili wanasema unapokuwa karibu na waridi lazima unukie, nataka niwahakikishie wananchi wa Igalula watanufaika na maji kutokana na ukaribu wa bomba hili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mimi kwenda katika Jimbo la Igalula, nipo tayari baada ya Bunge Mheshimiwa Mbunge kushirikiana naye kuhakikisha kwamba nakwenda kuzungumza na wananchi wa Igalula. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. GIBSON B. MEISEYEKI: Mheshimiwa Spika, nimpe pole Waziri kwa kupata shida kidogo na majina.
Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mkwamo mkubwa wa miradi ambayo Mheshimiwa Waziri ameitaja mingine hapa kutokana na urasimu wa malipo ya certificate kwa wakandarasi ambao wapo site. Miradi mingine imekwama kwa zaidi ya mwaka mmoja, mingine karibu miwili. Ni lini urasimu huu utakwisha ili miradi hii iweze kukamilika na kuwaondolea wananchi taabu hii ya maji ambayo imekuwa ni ya muda mrefu?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Kata zangu mbili za Odonyosambo na Odonyoas, wananchi kule wanataabika kwa kutumia maji yenye madini mengi, kwa maana hiyo wanapinda miguu na kuharibika kinywa nikiwa na maana meno yanaharibika kutokana na maji hayo na kwa sababu kuna chanzo ambacho Wilaya ya Longido wameki-abandon, wamepata chanzo kingine, ni lini Wizara sasa itaanza kuratibu kuwapelekea watu hawa ambao wanataabika kwa maji haya machafu ili kuwanusuru maisha yao na wananchi wengine waliopo pembezoni mwao waweze kufaidika na maji? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa maswali yake mazuri, lakini kikubwa ambacho nataka nilieleze Bunge lako Tukufu; sisi kama Serikali tumekuwa na utaratibu mpya wa kuhakikisha kwamba hatupeleki fedha tu, kwamba tunajiridhisha namna mkandarasi alivyofanya kazi kwa yeye ku-raise certificate, lakini kunakuwa na muda maalum, halmashauri inajiridhisha, mkoa unajiridhisha na sisi kama Wizara tunajiridhisha kazi bora iliyofanywa na mkandarasi.
Mheshimiwa Spika, lakini katika kipindi hiki cha uvumilivu au cha kusubiri, yawezekana akaona kama kuna suala la urasimu, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama kuna certificate ambayo imekuwa-raised na inahitaji kulipwa, baada ya Bunge naomba tukutane katika ofisi yangu ili tuhakikishe kwamba tunawasimamia ili wananchi wa Arumeru Magharibi waweze kupata maji ya uhakika na salama kama lengo la Serikali ilivyokuwa imepanga…
Mheshimiwa Spika, katika swali la pili amezungumzia suala zima la wanachi kupinda mifupa kutokana na fluoride. Sisi kama Serikali lengo letu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji, si maji tu, ni maji safi na salama. Kwa hiyo, sisi kama Serikali tumetengeneza maabara pale Arusha kuangalia teknolojia ambayo tunaweza tukapunguza fluoride, lakini pia kama Wizara tumejipanga kuangalia namna gani tunapata vyanzo vyenye mserereko ili visiwe na fluoride ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanakuwa salama na wanakuwa na afya bora. Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwanza hatudaiwi senti tano kutoka kwenye halmashauri yake, fedha zote tumeshalipa.
Mheshimiwa Spika, pili, tunaendelea kuhakikisha kwamba tuna-tap maji kutoka Mlima Meru na kuwapelekea wananchi wake na kwamba hadi sasa hakuna mwananchi hata mmoja anayeteseka kwa kukosa maji yaliyo safi na salama. (Makofi)
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa miradi mikubwa ya maji inachukua muda mrefu sana, ni kwa nini sasa Serikali haichimbi visima vifupi na virefu kwa kila mita 400 ili kupunguza adha ya maji kwa akinamama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, jambo lolote kubwa na jambo zuri lenye kuleta utekelezaji mkubwa na manufaa kwa wananchi lazima lichukue muda, lakini jambo litakalokuwa bora na lenye tija kwa wananchi. Kikubwa kuhusu suala zima la kuchimba visima vifupi; sisi kama Wizara tunafanya hivyo na tutaendelea kufanya hivyo ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata maji salama na yenye uhakika. Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, nitoe taarifa kwamba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango ametoa fedha maalum, Sh.3,900,000,000/= kwa ajili ya uchimbaji wa visima na fedha hizo tumekabidhi Mamlaka yetu ya Uchimbaji wa Visima na Ujenzi wa Mabwawa (DDCA). Kwa hiyo, tunaendelea kuchimba visima Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)
MHE. ZAINAB M. AMIR: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Kutokana na umuhimu wa mboga za majani kwa afya ya binadamu na ukizingatia maeneo mengi ya Dar es Salaam mboga hizo hulimwa mabondeni na kipindi cha mvua kuna mafuriko yanayoharibu mboga hizo. Je, ni lini Serikali itatenga maeneo maalum ambayo wakulima hawa watalima? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia wakulima hao mikopo ambayo itasaidia kulimo kilimo chenye tija na chenye kuzingatia afya ya mlaji? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, moja ya mikakati ya Serikali ni kuhakikisha kwamba inawatengea wananchi, hasa wajasiriamali wakiwemo wakulima wa mbogamboga na hili linafanywa na halmashauri au manispaa husika. Kwa hiyo ni suala zima la ufuatiliaji ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanaweza kupata maeneo sahihi ili wananchi wa Dar es Salaam waweze kunufaika na kilimo cha mbogamboga.
Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu suala zima la mikopo; bila ya nyezo huwezi kutoka, kuna namna bora ya kuhakikisha kwamba tunawasaidia wananchi wetu ili waweze kupata mikopo. Hili linatokana na halmashauri husika kwa kutenga asilimia tano za vijana na akinamama, ila kubwa sasa nimwombe Mheshimiwa Mbunge kushirikiana nao kusimamia fedha hizo ili waweze kupata na ziweze kuwasaidia wakulima wetu.
Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Nabu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ningependa kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Waziri utakubaliana na mimi kuvunwa kwa maji ya Mto Rufiji ni pasi moja ndefu mpaka golini, na ushindi huo unanufaisha akinamama kutua ndoo kichwani. Sasa ni kwa nini Serikali inapata kigugumizi kuanza kuyavuna maji haya ili kupoza kiu ya Mheshimiwa Rais ya kuwatua akinamama ndoo kichwani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa mradi huu hauna dalili ya kuanza leo wala kesho. Na kwa kuwa, mradi wa maji ya visima uliopo haukidhi mahitaji ya Wana Rufiji. Ni nini sasa kauli ya Serikali juu ya upatikanaji wa maji safi na salama ndani ya mita 400 kama ilivyo kwenye sera? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimpongeze dada yangu Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake wa Mkoa a Pwani na wananchi wa Rufuji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mpango wa Serikali kuutumia Mto Rufiji, nikubalianenae, kutumia Mto Rufiji kutaweza kuondoa tatizo kabisa la maji katika mji wa Rufiji, lakini kikubwa katika lengo na nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba, inawapatia wananchi wake maji. Si maji tu, ni maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa lengo na mkakati wa Rais wetu ni kuwatua ndoo akinamama kichwani na kwa kuwa hii ni Serikali ya Hapa Kazi Tu, kazi ya kuhakikisha kwamba mtaalamu mshauri kwa ajili mya kufanya upembuzi yakinifu wa/ya Mto Rufiji imeshaanza katika utaratibu. Kwa hiyo, subira yavuta heri, namuomba tusubiri kuhakikisha kwamba, tunatekeleza mradi ule wa Mto Rufiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili kuhusu suala zima la kuondoa tatizo la majni katika Mji wa Rufiji; ikumbukwe katika Bunge lako Tukufu katika Mji wa Rufiji tumetenga kiasi cha shilingi milioni 630,977,000 kwa ajili ya kuondoa tatizo la maji kwa kipindi hiki wanasubiri katika suala zima la kutumia Mto Rufiji. Ahsante sana.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ukiangalia majibu yaliyotolewa ni kwamba upembuzi unaendelea na gharama halisi zitajulikana Septemba.
Sasa hii inanipa wasiwasi kidogo kwa sababu kipindi hicho bajeti itakuwa imepitishwa, sasa wananchi wa Jimbo la Nkenge wawe na uhakika upi kwamba ni kweli mradi huu utaanza kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameeleza? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, tufuatane twende katika Wilaya ya Misenyi tuweze kupokea na kuona changamoto mbalimbali tunazokumbananazo katika utekelezaji wa miradi ya maji. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, lakini nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza Balozi kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya katika kuwatetea wananchi wake waweze kupata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wa Tanzania wanapata maji, na sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wake katika kuhakikisha wanapata maji, siyo maji tu, ni kwa maana ya maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahikishie wananchi wa Mheshimiwa Dkt. Kamala kwamba sisi katika bajeti yetu kwa kuwa tumeshakuwa na upembuzi, inatupa estimation cost ya kuwaweka katika suala zima la bajeti ili mradi huu uweze kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la kwenda kufanya ziara, nipo tayari kwenda kutembelea, siyo kwenda kuona tu katika hali ya kwenda kutatua matatizo ya maji katika Jimbo lake. Ahsante sana.
MHE. BONNAH M. KALUWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kutuletea maji Segerea, lakini nilitaka nimuulize Waziri, pamoja na kwamba tunapata maji asilimia 70, lakini kumekuwa na matatizo ya Kata kama Bonyokwa, Kipawa pamoja na Kiwalani na Minazi Mirefu. Sasa Serikali ina mpango gani kwa hizi Kata zilizobaki kuziletea maji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii, lakini kubwa napenda nitumie nafasi hii kumpongeza Mbunge wa Segerea kwa namna anavyowatetea wananchi wake. Moja ni Mbunge shapu ambaye alishafika ofisini kwetu katika kuhakikisha kwamba tunaenda kufanya ziara katika Mkoa wa Dar es Salaam katika Jimbo la Segerea. Sisi mpango wa Serikali ni kuhakikisha kuwapatia maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niko tayari baada ya Bunge kwenda kuongea na wananchi wa Segerea katika kufanya mpango wa haraka ili wananchi wake waweze kupata maji.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi.
Swali (a) kwa kuwa hapa ukiangalia tu haraka haraka kwenye jibu (a) unakuta kwamba kuna kazi kubwa inaendelea, lakini naomba hii kazi ukaone kwa macho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii Mlimba aliyosema Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa sasa inatumia maji ya kisima, kweli kuna kisima kimoja na hicho kisima kwa vile Mji wa Mlimba unakua kwa kasi na ni Makao Makuu ya Wilaya ya Tazara, yaani kwa wiki mara hii, moja, ndiyo maji tunapata. Kwa hiyo, naomba ukaone.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu sasa, kwa kuwa anasema kuna huu mradi ambao utakuja kufanyiwa upembuzi yakinifu kupata maji Mto wa Mgugwe na Mpanga, na kwa kuwa eneo la Mlimba lina vyanzo vingi vya mito, je, Serikali iko tayari kwenye huu mradi wa Mlimba kutumia maji ya Mpanga na Mgugwe kuingiza katika bajeti ya Serikali mwaka huu wa fedha ili wananchi wa Mlimba wapate maji safi na salama? (Makofi)
Pili, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumzia masuala ya Masagati, ni Kata ya Masagati; na hapa sitapoteza muda kusema mambo mengi, ninaomba sasa uje Mlimba maana umetoa ahadi nyingi sana hapa na Waheshimiwa Mawaziri wengi wakija wanaishia Ifakara badala kwenda Jimbo la Mlimba...
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki tukimaliza Bunge naomba Mheshimiwa Naibu Waziri twende Mlimba akaone hali halisi maana sasa hivi muda hautoshi kusimulia, ili akija hapa anapojibu maswali aone kama anajibu hali halisi kutokana na hilo Jimbo la Mlimba. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ukimwona mzee wa matobozano analia, ujue kuna jambo Mlimba. Kwa hiyo, mimi kama Naibu Waziri nipo tayari kwenda Mlimba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine kwa kuwa kuna changamoto kubwa sana Mlimba kwa ruhusa yako, namwomba Mheshimiwa Susan tuweze kukutana baada ya Bunge ili tuweze kuangalia namna pekee ya kuweza kuwasaidia wananchi wake. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza nianze kwa kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kufanya ziara katika Halmashauri ya Mbeya na katika ziara yake tuliahidi kuwa mradi wa Iwindi wananchi wangeanza kupata maji kabla ya Desemba mwaka 2017, je, ni lini mradi wa maji kwa Vijiji vya Izumbwe, Iwindi, Mwashiwawala na Mbalizi utakamilika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge wa Mbalizi, Mzee Njeza kwa kazi kubwa anayoifanya katika suala zima la kuhakikisha wananchi wake wanapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa nilishafanya ziara kule lakini ipo changamoto baadhi yetu wataalam kushindwa kusimamia miradi. Moja, nataka nimhakikishie tu, katika hali niliyoiona nipo tayari kushirikiana naye lakini pia na watalaam wetu kwenda katika kusukuma miradi ile ili wananchi wake waweze kupata maji kwa wakati. Ahsante sana.
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri maswali ya nyongeza kama ifuatavyo:-
(a) Je, ni lini sasa Serikali mtatimiza ahadi yenu na kutekeleza mradi huu wa Maji katika Mji ya Manispaa ya Kigoma Mjini kufika katika Mji Mdogo wa Mwandiga?
(b) Serikali haioni sasa ni muda muafaka maji haya ya Ziwa Tanganyika kwenda katika Wilaya ya Kasulu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa maji kwa Mji wa Mwandiga unategemeana kabisa na utekelezaji wa mradi huu mkubwa ambao utakamilika mwezi huu Disemba. Mradi huu utazalisha lita milioni 42 na mahitaji ya Mji wa Kigoma ni lita milioni 20. Kwa hiyo, kutakuwa na maji ya kiasi kikubwa ambayo tutaweza kuyapeleka katika Mji wa Mwandiga. Kikubwa nataka niwahakikishie wananchi wa Mwandiga subira yavuta kheri na kheri itapatikana katika upatikanaji wa maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili kuhusu suala la upatikanaji wa maji katika Mji wa Kasulu nataka nimhakikishie ndugu yangu Mheshimiwa Mbunge wali wa kushiba unaonekana kwenye sahani. Serikali imefanya kazi kubwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huu mkubwa wa maji, sasa hivi Mji wa Kasulu upo miongoni mwa miji 17 ambayo kupitia fedha za India utapata maji. Kikubwa tumsubiri Mhandisi Mshauri atatushauri vipi ili tupate maji ili kuhakikisha kwamba wananchi wa Kasulu wanapata maji kwa wakati. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Mafinga ni kati ya miji inayokuwa kwa kasi sana hapa nchi na hivyo uhitaji wa maji umekuwa ukiongezeka kwa kasi. Kutokana na jitihada mbalimbali ambazo wananchi wa Mafinga wanajituma na uwekezaji katika mazo ya misitu.
Je, Serikali, iko tayari lini kutupa kibali kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa miradi ya mwaka huu wa fedha wa 2017/2018?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, lakini nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Mheshimiwa Cosato Chumi kwa kazi kubwa anazozifanya na namna anavyofuatatilia ili wananchi wake wapate maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa Wizara imeshatoa kibali kwa mradi wa Mji wa Bumilianga ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi iliniweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri na pia nishukuru kwa kutupatia bilioni 1.66.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Maji katika Mji Mdogo wa Lushoto ilipatiwa fedha kwa ajili ya kujenga tenki la lita za ujazo 650,000 na banio katika eneo la Kindoi, lakini mpaka sasa mradi ule bado haujaanza. Nilifuatilia kwa Mkurugenzi wa Tanga UWASA alisema taratibu tushazikamilisha hivyo tunasubiri kibali kutoka Wizarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wamesubiri mradi ule haujaanza kwa muda mrefu sasa, naamini wananchi wananisikia na kuniona. Je, ni lini Mheshimiwa Waziri kibali hicho kitapatikana ili Mkandarasi aanze kazi mara moja, kwani mradi ule ukikamilika utaendelea kuhudumia Kata za jirani ambayo ni Ngulu na Ubiri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina vyanzo vingi vya maji pamoja na mito inayotitririka maji kutoka milimani. Je, Serikali ipo tayari kwa sasa kuhakikisha inatumia vyanzo hivyo pamoja na maji yanayotiririka kutoka milimani kujenga mabwawa na kutumia vyanzo hivyo ili kuwapatia wananchi wa Lushoto maji safi na salama na hasa kutimiza dhana nzima ya kumtua mama ndoo kichwani; hasa kina mama wa Kwekanga, Kwemakame, Mkuzi, Mazashai, Mazumbai, Ngwelo, Miegeo, Handei, Masange, Kwemashai, Gare pamoja na Magamba Coast? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Shekilindi kwa jinsi anavyofuatilia huduma ya maji katika Jimbo lake; na kwamba nishakwenda Lushoto, mazingira ya Lushoto ni mazuri, ni milima milima upo uwezekano mkubwa kabisa kuwapatia wananchi wa Lushoto maji safi na salama kwa zaidi ya asilimia mia moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza la Mbunge linahusu kibali, nitahakikisha kabla ya Bunge hili kukamilika kibali kitatolewa; kwa hiyo naomba sana tuwasiliane ili kibali kitolewe na utekelezaji wa mradi uendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, ni kweli kuna vyanzo vingi vya maji Lushoto na tutahakikisha kwamba tunaweka mabanio ya kutosha kule milimani na kuweka mabomba kwa sababu maji ni ya mserereko hayana gharama kubwa na pale itakapobidi tutajenga hadi mabwawa ili maji yawe ya kutosheleza.
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Niipongeze tu Serikali kwa jibu zuri lenye matumaini hasa kwa wananchi wa Manyoni wanaoishi katika Bonde la Ufa katika maeneo ya Unyambwa, Unyangwila na Mgunduko. Hata hivyo, nina swali dogo la nyongeza pamoja naombi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na ombi, naomba katika bajeti hii inayofuata ya 2018/2019 nione bajeti ya uchimbaji wa bwawa hili imetengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la nyongeza ni kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni imebainisha maeneo katika vijiji vitatu kwa ajili ya kuchimba mabwawa madogo. Vijiji hivi ni Makutupora, Winamila pamoja na Igwamadete. Je, Serikali itakuwa tayari kutuuunga mkono kama Halmashauri?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya kuwatetea wananchi wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa napenda nimueleze Mheshimiwa Mbunge, sisi ni Wizara ya Maji na jukumu letu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji. Nimhakikishie katika Bwawa lile la Mbwasa tutawaweka katika bajeti 2018/2019 ili kuhakikisha wananchi wake wanapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa lingine pamoja na jitihada ya kuainisha maeneo kwa ajili ya mabwawa, nataka nimhakikishie Serikali na Wizara yetu pamoja na wadau wa maendeleo tumekuwa tukishirikiana katika kuhakikisha tunachimba mabwawa maeneo yenye ukame. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo, tuko tayari kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge katika kuhakikisha maeneo yenye uhitaji wa mabwawa wanapata mabwabwa ili waondokane na ukame kwa kupata maji. (Makofi)
MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali imesema kwamba itaunda timu maalum kwa ajili ya kushughulikia suala hili la Mtawango, lakini Kamati ya LAAC ilituletea taarifa yake hapa Bungeni ambayo ilionesha kwamba kuna ufisadi mkubwa unaoendelea katika miradi mbalimbali ya maji hapa nchini. (Makofi)
Je, Serikali ipo tayari kuunda Tume ya Kitaifa itakayoweza kuchunguza miradi mbalimbali ya maji hapa nchini na kutuletea taarifa ya ripoti yake hapa Bungeni kama ambavyo Kamati ya LAAC ilipendekeza?
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Ng’apa wa maji safi na salama ambao uko Lindi uliopelekea hadi Rais akamtumbua na kumfukuza nchini yule mhindi mpaka leo hii haujakamilika na kusababisha wananchi wa Lindi kukosa maji salama na safi.
Je, ni kwa nini mradi huu mpaka leo hii haujakamilika pamoja na kuwepo na maagizo ya Rais? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni maelekezo ya Kamati ya LAAC ambayo yaliweka maazimio ya kuunda mpaka Tume kuhusu kuchunguza miradi ya maji, kwa sababu tayari maazimio hayo yalikubalika na Bunge nafikiri hebu tuyaache sasa, hayo maazimio yaweze kufanyiwa kazi badala ya kuunda tume nyingine ya pili.
Swali la pili, ameulizia kuhusu Mradi wa Ng’apa nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi wa Ng’apa umekamilika na sasa hivi unatoa maji Mjini Lindi, kama una ndugu zako wako Lindi kule naomba uwapigie simu, tayari mradi umekamilika na nimetoa tena fedha shilingi milioni 500 ili tuweze kuweka miundombinu ya kusambaza maji Mjini Lindi ili maeneo mengi yaweze kufaidika na mradi wa Ng’apa.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi naomba nimshukuru pia Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na naomba tu niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, vijiji hivi 100 kimsingi ni ahadi iliyotolewa na Serikali mwaka 2014 hapa Bungeni na ilitegemewa kufika mwaka 2015 vingekuwa vimepata huduma ya maji, lakini mpaka sasa hivi kama ambavyo jibu limeeleza kwamba fedha hazijapatikana.
Nilitaka nipate tu uhakikisho wa Mheshimiwa Waziri, kwamba kwa mwaka huu wa fedha tunaouanza 2018/2019 je, Serikali inaweza ikamaliza hii ahadi ya muda mrefu ili vijiji hivyo vipate maji?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hivi sasa Serikali inatekeleza miradi miwili mikubwa ya maji. Mmoja ni wa maji kutoka Kahama kwenda Isaka na mradi mwingine ni wa kutoka Mangu kwenda Ilogi. Miradi hii yote inatekelezwa kwa awamu ya kwanza kwa maana ya kupeleka bomba kuu peke yake bila usambazaji kwenye vijiji vilivyo jirani. Ahadi imekuwa kwamba awamu ya pili ambayo itaanza 2018/2019 itahusisisha usambazaji wa maji kwenye vijiji vilivyo jirani.
Je, Waziri anaweza akanihakikishia kwamba utekelezaji wa hii awamu ya pili ambayo itahusisha usambazaji wa maji kwenye vijiji vilivyo jirani katika miradi hiyomiwili utatekelezwa pia?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba awali ya kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anazozifanya katika jimbo lake na kuwatetea wananchi wake wa Msalala.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kabisa ahadi ni deni na hii ni ahadi ya Serikali. Nataka nimuhakikishie kwamba katika vile vijiji 100 sisi kama Wizara ya maji tulikuwa tukitoa fedha na tutaendelea kutoa katika kuhakikisha vijiji vinapatiwa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu katika vijiji ambavyo vipo katika awamu ya pili, tunatambua siku zote safari yoyote ni hatua. Tumeshaanza hatua ya kwanza katika kuhakikisha kwamba tunaliweka bomba kuu, na tutahakikisha kwamba baada ya kukamilika utandazaji wa bomba hili kuu vijiji vilivyokuwa jirani ya kilometa 12 vyote vitapatiwa maji; ahsante sana. (Makofi)
MHE ABDALLAH A. MTOLEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la maji liliko Msalala linafanana na tatizo la mji liliko katika Halmashauri ya Temeke ambayo kwa kiasi haina mfumo wa maji ya bomba. Hata hivyo bomba kubwa la maji kutoka Mto Ruvu linalopeleka maji katika Kambi ya Jeshi ya Navy linapita Temeke.
Sasa ni lini Serikali itatoa matoleo kutoka kwenye bomba lile ili wananchi wa Kata za Mtoni, Azimio, Tandika, Makangarawe pamoja na Buza nao waweze kupata maji kutoka kwenye bomba hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri, lakini nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jukumu la kuwapatia wananchi maji ni jukumu letu sisi Wizara ya Maji na kwa kuwa sisi ni Wizara ya Maji na si Wizara ya ukame tupo tayari kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. Mheshimiwa Mbunge nataka nikuhakikishie Jumatatu mimi naanza ziara katika mkoa wa Dar es Salaam, na katika maeneo nitakayotembelea nitafika Temeke tuangalie namna bora ya kuweza kuwapatia wananchi wako maji. Ahsante sana.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Kabla ya yote nipende kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano ya Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutupatia mradi huu mkubwa wa kutuletea maji safi na salama kwa ajili ya binadamu na mifugo toka Mlima Kilimanjaro Mto Simba.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa wananchi wa hizi Kata tatu zilizolengwa na mradi huu wana shauku kubwa ya kupata maji haya ikizingatiwa kwamba Wilaya hii ni kame, Je, mradi huu unategemewa kukamilika lini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kufahamu uhaba wa maji katika Wilaya ya Longido Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji alipotembelea Longido mwaka jana aliwaahidi wananchi wa Kijiji cha Wosiwosi wanaoishi pembezoni mwa Ziwa Natron lenye maji yasiyofaa kwa matumizi ya binadamu pamoja na wananchi wa Kata ya Tingatinga katika Kijiji cha Tingatinga kwamba atawapatia mabwawa ya maji; je, ahadi hii ataitimiza lini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ya kipekee anavyowatetea wananchi wake wa Longido. Kubwa tu itambulike kutokana na changamoto kubwa sana kwa Mji ule wa Longido katika suala zima la maji, Wizara yetu ikaona haja ya kuwapatia wananchi wale maji safi na salama na ya kuwatosheleza, lakini anataka kujua ni lini mradi ule unakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi ule unakamilika mwishoni mwa mwezi Mei. Mimi kama Naibu Waziri nilipata nafasi ya kufika pale katika kuhakikisha tunausukuma mradi ule ili wananchi waweze kupata maji safi na salama. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, nilipofika katika ule utekelezaji wa mradi nimemkuta Mkandarasi amelala, nilimtikisa kwa mujibu wa mkataba ili mwisho wa siku wananchi wake wapate maji. Nataka nimhakikishie tutashirikiana ili wananchi wake waweze kupata maji safi na salama kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la ahadi ya Mheshimiwa Waziri ya mabwawa, nataka nimhakikishie ahadi ni deni. Sisi kama Wizara ya Maji kwa kuwa Mheshimiwa Waziri ameahidi tutatekeleza kwa wakati katika kuhakikisha wananchi wake wanapata maji.
MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Kambi Mbadala, kwanza niwapongeze Wizara hii ya Maji kwa kufanya kazi vizuri hasa mdogo wangu kwa kubeba ndoo kichwani. Kule Mnyuzi katika Kijiji cha Lusanga kuna mradi mkubwa wa maji ambao upembuzi yakinifu umeshafanyika na maji hayo yangeweza kufika mpaka Shamba Kapori; je, mradi huu mpaka sasa hivi umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana. Hata hivyo, nimpongeze Kaka yangu Mheshimiwa Maji Marefu kwa namna anavyowapigania wananchi wake wa Jimbo la Korogwe Vijijini. Nataka nimhakikishie yeye ni jembe wembe!
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa kama alivyokuwa amesema, upembuzi yakinifu umeshakamilika, kubwa nimwombe tu Mhandisi wa Maji wa Korogwe Vijijini asilale. Ahakikishe kwamba anatangaza ile kazi ili mwisho wa siku Mkandarasi apatikane na utekelezaji wa mradi uanze mara moja na Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo katika kuhakikisha tunawapa fedha ili mradi ule ukamilike kwa wakati. Ahsante sana.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza niipongeze Serikali kwa mkakati mkubwa inayoweka kuhakikisha wananchi wote kwenye vijiji wanapata maji. Hata hivyo, tukirudi nyuma historia ni kwamba Serikali ilipochimba visima iliachia Kamati za Maji kuendesha visima hivyo. Je, Serikali kwa sababu imejizatiti kupeleka maji kila kata na vijiji, ina mpango gani ya kuchukua wale wanafunzi wenyeji waliomaliza Kidato cha Nne wakajifunze Chuo cha Maji kwa ajili ya kuja kusimamia visima hivyo ili viweze kutumika kwa muda mrefu. Mheshimiwa Naibu Spika, ni hilo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge, mama yangu, kwa swali zuri, lakini kikubwa na sisi tumepokea ushauri. Tulivyoanzisha miradi ya maji na kuhakikisha wananchi wanapata maji, lakini lazima kuwe na usimamizi, tukaona haja ya kuwashirikisha wananchi katika kuhakikisha kwamba, kunakuwa na jumuiya za watumiaji maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na nia njema ya kuweka jumuiya ya watumiaji maji, lakini kumekuwa na changamoto za aina yake. Sisi kama Wizara ya Maji tumekuwa na Chuo cha Maji kipo pale Ubungo; ni fursa pia niwahamasishe vijana wenzangu wapate nafasi ya kufika pale na sisi kama Wizara tutaangalia namna ya kuweza kuwasaidia katika kuhakikisha na wao wawe sehemu ya kumiliki miradi ile ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini shida ya ya maji Longido ni sawasawa na shida ya maji iliyopo Jimbo la Igalula. Maeneo mengi ya Jimbo la Igalula maji chini hayapatikani kwa urahisi, visima vingi vimechimbwa lakini havitoi maji na kusababisha kupotea fedha nyingi za Serikali; lakini yako maeneo mengi ambayo yanaweza yakachimbwa mabwawa na yakasaidia upatikanaji wa maji katika Jimbo la Igalula.
Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti umeshafanyika, upembuzi yakinifu na usanifu katika Kata ya Goweko na Igalula umeshafanyika, lakini mpaka sasa miradi hii haijafanyika na miradi hii ilikuwa kwenye bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/2017, lakini mpaka sasa hakuna kinachofanyika. Sasa naomba kujua miradi hii ni lini itatekelezwa? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru. Moja tu, ukimwona mtu mzima analia ujue kuna jambo. Sasa mpaka Mheshimiwa Ntimizi analia maana yake Igalula kuna hali mbaya sana katika suala zima la maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji na kwa kuwa, sisi si Wizara ya ukame, tupo tayari kushirikiana nae katika kuhakikisha tunawachimbia mabwawa ili wananchi wake waweze kupata maji kwa wakati. Ahsante sana.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa NJaibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, mradi huu umechukua muda mrefu sana. Ukiangalia kwenye swali la msingi ni tangu 2008, lakini ukija kwenye majibu anasema usanifu umekamilika tangu 2013. Pamoja na kwamba Serikali inasema wako kwenye evaluation wananchi wa Wilaya ya Moshi na hususan wa Kata ya Tela wanataka kujua, huu mradi umetengewa shilingi ngapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; katika Wilaya ya Serengeti kuna miradi ya maji kwenye Vijiji vya Nyagasense, Rung’abure na Kibanchebanche. Mradi wa Nyagasense hautoi maji na walishalipa retention yote. Pia Mradi wa Rung’abure hautoi maji. Mradi wa Kibanchebanche mkandarasi ametokomea na nimemwambia Mheshimiwa Waziri twende Serengeti, hatukwenda mpaka leo, wameshalipa mpaka retention lakini miradi haitoi maji. Ni nini tamko la Wizara dhidi ya matatizo haya ambayo yametokea, wamelipwa fedha zote miradi haitoi maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimjibu swali kaka yangu Mheshimiwa Marwa Chacha, moja alitaka kujua gharama ya mradi; gharama ya mradi itagharimu kiasi cha milioni mia nane ishirini na mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili; kuna baadhi ya miradi ambayo imeshalipwa fedha za Serikali lakini haitoi maji. Nataka nimhakikishie sisi kama Wizara ya Maji na kama viongozi; maana unapokuwa Naibu Waziri, ni jukumu lako kuhakikisha wananchi wanapata maji. Sisi hatutamwonea haya yeyote ambaye amefanya ubadhirifu wa fedha za Serikali. Kama kweli kuna fedha ambazo kuna mtu amezila, basi ajiandae kuzitapika ili wananchi waweze kupata maji. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa hali ya kusuasua kwa huu mradi wa Mande, Tela kunafanana kabisa na miradi mingine iliyo katika maeneo ya tambarare ya Mkoa wa Kilimanjaro, ukiweko ule mradi wa Mwanga mpaka kule Hedaru mpaka Mombo. Ni lini sasa Serikali itatupa muda muafaka wa kukamilika kwa miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru. Tunapozungumzia suala la maji, maji hayana mbadala, si kama wali, ukikosa wali eti utakula ugali. Kwa hiyo kuna haja kubwa sana ya kuhakikisha wananchi wanapata maji kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi kama Wizara ya Maji katika kuhakikisha wananchi wanapata maji kwa wakati lazima kuwe na ufuatiliaji na usimamizi wa karibu. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga katika kufuatilia na kusimamia miradi hii kwa wakati ili wananchi waweze kupata maji kwa muda muafaka uliopangwa. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Naomba niipongeze Wizara na Serikali kwa kutengea fedha Mradi wa Endasak, Endagao na Endeshwal na Mradi wa Malama.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hivyo miradi hii miwili imepangiwa shilingi bilioni 1.31 na bilioni 1.2 mradi wa pili na naishukuru Serikali kwa kuanza kutekeleza mradi, lakini imechukua muda mrefu sana. Naomba kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini kasi itaongezeka ili miradi hii miwili iweze kukamilika kwa sababu Wilaya ya Hanang ilivyo chini ya Rift Valley ina ukame na watu wanapata shida kubwa sana ya kutafuta maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Mary Nagu, mama yangu kwa namna anavyowapigania wananchi wake. Kubwa ni kwamba sisi kama Wizara ya Maji jukumu letu ni kuwapatia wananchi maji. Zipo changamoto ambazo tumekumbana nazo, moja ni wakandarasi ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa kusuasua.
Mheshimiwa Naibu Spika, labda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara tumejipanga kwa mkandarasi ambaye atatuchelewesha katika kuhakikisha wananchi wanapata maji, hatuna sababu ya kujadiliana naye, tutamwondoa, tutamweka mtu ambaye ataweza kufanya kazi kwa wakati ili wananchi waweze kupata maji kwa muda uliopangwa. Ahsante sana.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina swali moja au mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni imani yangu kwamba dhamira ya Serikali ni kuwahudumia wananchi na kuwapelekea huduma iliyo imara, lakini swali la msingi ilikuwa ni kueleza changamoto ya miradi hii.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kufanya ziara kupitia miradi yote ambayo nimeitaja hapo juu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mwenda kwao haogopi kiza na Kilindi ni nyumbani, nipo tayari kwenda Kilindi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kila tunapouliza kuhusu ukarabati mkubwa wa Mradi wa Makonde tunaambiwa kwamba kuna dola za Kimarekani milioni 84 ambazo ni za mkopo kutoka Serikali ya India, lakini kila siku tunaambiwa majadiliano yanaendelea. Sasa nilitaka nipate commitment ya Serikali, majadiliano hayo yataisha lini na mkataba utasainiwa lini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, mradi huu wa Makonde unahusisha Halmashauri nne; Newala Vijijini, Newala Mjini, Tandahimba na Nanyamba, lakini majibu ya Naibu Waziri yanazungumzia Halmashauri tatu tu. Sasa nilitaka nipate maelezo ya Serikali kuhusu mpango wa Serikali kutoa maji Mitema na kupeleka Halmashauri ya Mji wa Nanyamba.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Chikota kwa namna ya kipekee anavyowatetea wananchi wake, lakini kikubwa ni kuhusu suala la fedha za India.
Sisi kama Wizara ya Maji, kwa kuwa huu ni mpango mkubwa na mpango wowote mkubwa wenye mafanikio makubwa lazima uchukue muda. Sisi kama Wizara tunafuata taratibu lakini tunaamini utekelezaji wa mradi huu utaondoa kabisa tatizo la maji. Kwa hiyo, sisi kama Wizara ya Maji tutafanya jitihada za haraka ili jambo hili liweze kukamilika.
Mheshimiwa Spika, kuhusu suala zima la chanzo cha Maji cha Mto Mitemba, sisi kama Wizara tumeshapokea andiko kuhusu suala zima la kutumia chanzo cha Mitemba ambacho kitaweza kutatua tatizo la maji kwa Halmashauri tatu, kwa maana ya Halmashauri ya Tandahimba, Newala na Nanyamba pamoja na maeneo ya jirani. Kwa kuwa andiko lile tumelipata, tunalifanyia kazi katika kuhakikisha tunalitekeleza kwa wakati kama ilivyopangwa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FELISTER A BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maporomoko ya Ntomoko ni janga kwa wananchi wanaoishi kandokando ya maporomoko haya. Wananchi wa Wilaya ya Chemba vijiji kumi na vijiji vitatu vya Wilaya ya Kondoa wamesubiri mradi huu kwa muda mrefu sana na fedha zilishatolewa zaidi ya bilioni mbili kwa ajili ya kukarabati mradi ule, watumishi ambao walizembea mradi ule hawajachukuliwa hatua yoyote. Wananchi wanateseka na hakuna jibu lolote linaloonesha kwamba hivi vijiji vitapata maji hivi karibuni.
Je, watumishi waozembea na wakapoteza zaidi ya shilingi bilioni mbili na kufanya mradi huu ukasimama wamechukuliwa hatua gani?
Swali la pili, mradi huu umekwishatembelewa na viongozi wengi na tumekwishachangia mara nyingi na Wabunge wa maeneo yale mimi na Mheshimiwa Juma Nkamia na Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji sasa hivi hatueleweki kwa wananchi.
Je, kuna mkakati gani wa haraka wa kuwapatia wananchi wa vijiji vile maji ili wasiendelee kuhangaika kwa sababu hata DUWASA wenyewe hawajapata fedha kwa ajili ya ule mradi? (Makofi)
NAIBU WA WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimpongeze Mama yangu Felister Bura kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ambalo nashukuru sana ni taarifa ambayo amenipa kama Naibu Waziri wa Maji, nataka nimhakikishie fedha za Serikali haziliwi bure. Kama kutakuwa na watumishi ambao kwa kuzembea au kwa maksudi fedha zile zimepotea, tutafanya mawasiliano ya haraka na watu wa Kondoa katika kuhakikisha hatua za haraka zitachukuliwa kwa watumishi wale ambao wamefanya uzembe wananchi waweze kupata taabu.
Swali lake la pili, amesema huu ni mradi wa muda mrefu sana nataka nimuhakikishie sisi ni Wizara ya Maji na jukumu letu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama yenye kuwatosheleza na ndiyo maana tumeahidi kwamba katika bajeti hii ya mwaka 2018/2019 tumeshatenga fedha ili katika kuhakikisha mradi ule uweze kukarabatiwa kwa haraka ili wananchi wake waweze kupata majisafi salama na ya kuwatosheleza. Ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba kumfahamisha Mheshimiwa Felister Bura kwamba kuna hatua za dharura ambazo tunaendelea nazo, tunachimba visima katika vijiji vyote eneo la Kondoa na tumeshaanza na visima 15 ili wananchi waendelee kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, ni lini Serikali itasaini mkataba huu wa Euro milioni 70 maana toka mwaka 2017 tunaambia itasaini. Sasa tunataka kujua ni lini Serikali itasaini mkataba huu ili wananchi wa Morogoro wapate maji? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Morogoro Mjini kuna mgao wa maji, mwananchi anaweza akakaa miezi mitatu hajapata maji lakini cha ajabu analetewa bili ya maji mwisho wa mwezi ili aweze kulipa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake, ni namna gani jinsi anavyowapenda. Mimi nataka niwahakikishie wananchi wa Morogoro hawakukosea kumpata Mbunge huyu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kubwa mimi kama Naibu Waziri nilifika Morogoro na niliona hali ya upatikanaji wa maji katika Mji ule wa Morogoro na namna gani wananchi wanavyolalamika kuhusu suala zima la maji. Anataka kujua ni lini sasa tutakaposaini mkataba ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana hasa katika suala zima la fedha na suala la fedha lazima lifuate taratibu zake. Sasa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa maji hayana mbadala, si kama wali ukikosa wali utakula makande au ugali kuna haja ya haraka kuwapatia wananchi wake maji na sisi kama Wizara ya Maji tutafanya jambo hilo haraka ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la bili nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kutokana na changamoto hiyo Waziri wangu aliitisha kikao cha Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Maji nchini katika kuhakikisha wanajadili changamoto hii ya maji na akawapa maelekezo. Nataka niwaagize tena Wakurugenzi wote. Maagizo ambayo ametoa Waziri kuhusu suala zima la kutokuwabambikia wananchi bei lazima watoe bei ambazo zimeidhinisa na EWURA na yale maelekezo ambayo yanahusu suala zima la bei wafanye kama walivyoelekezwa.
Mheshimwia Mwenyekiti, kama kuna Mkurugenzi atakayekaidi atakavyoenda ndivyo sivyo atuharibie sisi kazi tutamharibia yeye kabla ya sisi kutuharibia. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililoko Morogoro Mjini halina tofauti na tatizo lililopo Manyoni Magharibi. Wananchi wa Jimbo la Manyoni Magharibi kwa muda mrefu wamekuwa wakihangaika na kero kubwa ya ukosaji wa maji safi na salama na maeneo yaliyoathirika ni Itigi Mjini, Songareli, Mlowa, Tambukareli, Majengo na Zignal.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wananchi wa Jimbo la Manyoni Magharibi maji safi na salama na kuwatua ndoo wanawake? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge na si mara moja amenieleza kuhusu suala hili, mambo mazuri hayataki haraka. Kwa kuwa sisi Wizara ya Maji si Wizara ya ukame tarehe 7 Mei, 2018 tunawasilisha bajeti yetu ya Wizara ya Maji; kwa hiyo namuomba sana tuwe katika suala zima la subira na subira yavuta heri, heri itapatikana katika kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. Ahsante sana, itatekelezeka. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali fupi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Manispaa ya Morogoro licha ya mipango mizuri ya Serikali imekuwa na matatizo kweli ya maji. Je, kuna mkakati gani wa kuanzisha vyanzo vingine vya maji katika Manispaa ya Morogoro ikiwa ni mkakati wa muda mfupi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji halisi kwa sasa ya Mji wa Morogoro ni lita 45,000 mita za ujazo kwa siku, lakini Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (MORUWASA) yanatoa maji 34,000 lita za ujazo kwa siku; kwa hiyo kuna uhaba katika suala zima la maji. Serikali kwa kuona haja ya kuongeza kiwango cha maji ndiyo maana tupo katika utaratibu wa kusaini Euro milioni 70 katika kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo la maji katika Mji wa Morogoro.
MHE. KHADIJA HASSAN ABOUD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na nina swali dogo kwa Mheshimiwa Naibu Waziri.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha katika Halmashauri zote hawa mawakala wa maji, pre-paid meter ili kuepusha wananchi kubambikiziwa bili na kuepusha wananchi au taasisi kutokulipa bili za maji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Wizara ya Maji ni katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na mpango wa kisasa kuwa na pre-paid meter. Mpaka sasa Mheshimiwa Waziri ameshaziagiza mamlaka hizo zifungwe na mpaka sasa zipo mamlaka saba ambazo zimeshaanza kutekeleza mradi huo. Kwa zile mamlaka ambazo bado hazijatekeleza lazima watekeleze katika kuhakikisha tunaondoa tatizo hilo.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kata ya Msongola, Chanika, Zingiziwa, Buyuni na Pugu hazina maji; na kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri wa Maji alisema kuwa Mradi wa Kimbiji na Mpera ukikamilika ndio utaleta maji Ukonga. Ningeomba nijue mpaka sasa mradi huu umefikia katika hatua gani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyowapigania wananchi; lakini kubwa sisi tulifanya ziara katika Mkoa wa Dar es Salaam na nimefika hadi katika maeneo yake. Jitihada kubwa ambayo Serikali inaifanya mpaka sasa ni kuchimba visima 20 kwa maeneo ya Kimbiji na Mpera katika kuhakikisha wanapeleka maji maeneo yale. Hata hivyo kikubwa sasa hivi katika utekelezaji wa mradi ule lazima tusambaze kwa kutegemea na fedha. Kwa hiyo, tupo katika jitihada ya kutafuta fedha ili tuweze kutekeleza mradi ule na kuweza kuondoa tatizo la maji katika maeneo ya Ukonga. (Makofi)
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tafsiri ya swali langu, nilipenda kujua miradi ambayo inatekelezwa katika Mkoa wangu wa Ruvuma mimi kama mwakilishi wa mkoa ule, lakini majibu ya Mheshimiwa Waziri yameeleza kwamba kuna miradi ambayo inatekelezwa katika vijiji 230, vimekamilika vijiji 94.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kunisaidia kujua miradi hiyo ipo katika maeneo gani? Mimi kama mwakilishi wa wanawake wa Mkoa wa Ruvuma nipate kujua ni ipi inatekelezwa ili nilete msukumo katika Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, ipo maradi miwili sugu ambayo inatekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru. Kuna Mradi wa Mtina na Mradi wa Matemanga. Miradi hii ni ya muda mrefu sana na ilitakiwa iwe imekamilika. Hivi ninavyozungumza, Halmashauri imesitisha mikataba ya wale wakandarasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama inavyofahamika ni kwamba tafsiri ya wananchi ni kuona miradi inakamilika na inatoa maji. Je, nini kauli ya Serikali katika kuhakikisha miradi hii inakamilika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyowapigania wananchi wake, Mwenyezi Mungu ambariki sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wangu aliniagiza kwenda Mkoa wa Ruvuma kufanya ziara na kuangalia hali ya upatikanaji wa maji. Pamoja na kuangalia, nilijiridhirisha kupita katika Halmashauri zote za Mkoa wa Ruvuma, lakini kuna kazi kubwa sana inayofanyika katika vijiji mbalimbali. Moja, Ngunguru, Mbesa, kuna Chandarua, Jeshini na Muungano, yote kuna sehemu ya utekelezaji wa miradi ya maji. Kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge anataka kujua vijiji vyake kwenye utekelezaji wa maji, nipo tayari baada ya Bunge nimpe nyaraka hii ambayo imeidhinisha vijiji vyote ambavyo utekelezaji wa maji upo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, kumekuwa na kusuasua sana kwa miradi ya maji kwa mfano Matemanga. Mimi Naibu Waziri nilifika pale kuona hali ya upatikanaji wa maji, lakini tumekuja kujifunza kwamba pamoja na Serikali kupeleka fedha, lakini kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa sana wakandarasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya sababu ni watu kupeana kazi kishemeji shemeji au kiujomba jomba. Kwa hiyo, kwa kuwa kazi ya Waziri au kazi ya Wizara yetu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji, tumeiomba Halmashauri isitishe mkataba na yule mkandarasi, watafute mkandarasi mwingine haraka ili wananchi wale waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili bwawa mwaka 2017 liliharibika spillway. Spillway ilikuwa upande wa mashariki mwaka 2016/2017 ikaharibika ile ambayo ilikuwa upande wa mashariki na mkandarasi akairekebisha akaiweka upande wa magharibi ambayo mwaka huu imeharibika. Sasa Serikali inasemaje kuhusu hilo na kuwahakikishia wananchi wa sehemu hizo kwamba spillway haitaharibika tena baada ya kuikarabati mwaka huu? La kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, bado niko kwenye maji Chunya Vijijini; Mji Mdogo wa Makongorosi una watu zaidi 20,000 na una uhaba sana wa maji. Hata ule mradi wa maji visima kumi kila kijiji Makongorosi walikosa maji. Sasa hivi wananchi wa Makongorosi pamoja na Mbunge wao, wamechimba kisima kwenye kijiji cha Ujerumani. Kisima kina maji mengi sana lakini hakina miundombinu ya kuweza kutoa maji hapo kuyapeleka kijijini.
Je, Serikali iko tayari kusaidia mradi huo ili kumtua mwanamke ndoo kichwani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri inayoifanya katika Jimbo lake. Kama nilivyoeleza kuhusu suala la kuharibika kwa spillway, sisi kama Wizara ya Maji tunatoa fedha katika kuhakikisha wananchi wale wanapata mradi uliokuwa bora ambao utaweza kuwahudumia wananchi kwa muda mrefu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa sasa ni kipindi cha pili mradi huo unaharibika, labda nitatuma timu ya wataalamu wetu wa Wizara kwenda kuhakikisha mradi ule ili mwisho wa siku ukamilike kwa wakati, lakini mradi utakaokuwa bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, Swali la pili kuhusu yeye pamoja na wananchi wake kuchimba kisima, lakini bado kumekuwa na changamoto ya miundombinu ya kuwafikiwa wananchi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie sisi kama Wizara ya Maji hatututakuwa kikwazo katika kumsaidai yeye pamoja na wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. Kubwa nimwombe Mhandisi wa eneo hilo achangamke, asilale. Alete mchanganuo tuangalie namna gani tunaweza tukamsaidia ili wananchi wake waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mwaka jana niliuliza swali kuhusiana na bwawa la Mwamihanza nikaambiwa Serikali inatafuta fedha; mwaka huu pia nimeuliza juu ya miradi hii ya umwagiliaji kwenye vijiji hivi vitatu majibu ya Serikali ni kwamba bado Serikali inatafuta fedha. Sasa nataka kuiuliza Serikali, pesa itapatikana lini? Kwa sababu kwenye Bwawa la Masela usanifu ulishafanyika na watu walishaondolewa kwenye eneo ambalo bwawa litachimbwa. Sasa Serikali inapata pesa lini ili kuanza ujenzi wa Bwawa la Masela?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Tume ya Taifa ya Umwagiliaji inapata pesa kidogo sana, ndiyo maana miradi mingi ya umwagiliaji inakwama. Mradi wangu wa Bukangilija umekwama wa Mwatigi umekwama wa Kulimi umekwama sasa ni lini Serikali itatenga kiasi cha fedha cha kutosha ili kushughulikia miradi ya umwagiliaji hapa nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze kwanza Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyofanya kazi. Pili, amezungumzia kuhusu suala la uchache wa fedha na lini Serikali itatoa fedha. Pamoja na Serikali kutoa fedha lakini kupitia ziara tulizokuwa tumezifanya tumeona katika miradi mingi ya umwagiliaji kumekuwa na changamoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, tuna miradi ya zaidi ya 889 ambayo imejengwa lakini miundombinu yake haijakamilika, lakini la pili ipo miradi 54 ambayo imejengwa lakini haifanyi kazi kabisa. Kutokana na changamoto hiyo Waziri wangu akaona haja ya kupitia mpango kabambe wa mwaka 2002 wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili kuangalia namna gani tutaweza kutumia fedha ingawa kwa uchache lakini miradi iwe yenye tija. Nataka nimhakikishie kupitita mapitio haya tuliyoyafanya miradi ile ambao tumeiorodhesha na tumeibainisha ipo haja ya kutengeneza maaboreshe na ili hata kama miradi inatekelezawa lazima iwe miradi ambayo imekamilika kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu miradi yake ambayo ameelekeza, katika miradi ambayo tumeanisha na yeye tutamuweka katika utekelezaji ili miradi iende kwa wananchi kama zamani. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Maji mengi sana ya mvua yanapotea katika nchi hii kiasi kwamba tungekuwa na utaratibu wa kuyavuna yangeweza kusaidia katika shughuli za umwagiliaji na shughuli za wanyama. Kwa mfano katika Jimbo langu la Rombo kuna mito ya msimu kama Ungwasi, Marwe, Tarakea, Uashi pamoja na Nana ambapo maji ya mvua ambayo yanakwenda nchini Kenya wale wameyazuia wanafanya nayo umwagiliaji halafu wanatuletea tena bidhaa huku kwetu.
Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari utakapopata nafasi twende wote Rombo ukayaone haya mabonde ya mito hii ya msimu ili tuweze kuangalia uwezekano wa kuyazuia ili tuweze baadae kuyatumia kwa ajili ya umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Selasini Mzee wangu, mimi kama Naibu wa Waziri wa maji nipo tayari baada ya Bunge twende pamoja Rombo ahsante sana. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza; katika Wilaya ya Karatu mkoa wa Arusha kijiji cha Mang’ola kuna biashara kubwa ya kimataifa ya vitunguu ambapo robo ya mapato ya Halmashauri ya Karatu yanatokana na kilimo hiki cha vitunguu.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea mabwawa na mifereji ya umwagiliaji wananchi hawa wa Mang’ola ili kuongeza tija kuwainua kimaisha wananchi wa Karatu hasa akina mama waliowekeza katika kilimo hiki cha vitunguu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu asilimia kubwa zaidi ya 70 wanaishi vijijini na wanategemea kilimo cha kudra za Mwenyezi Mungu kwa maana ya mvua. Kwa hiyo sisi kama Wizara ya Maji tukaona haja sasa ya kuwa na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika kuhakikisha kilimo chetu kinakuwa bora na tija katika suala zima la uzalishaji, kwa maana ya kupata malighafi za viwandani na hata katika suala zima la biashara. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo katika kuhakikisha tunatengeneza miundombinu ya umwagiliaji eneo hilo ili wananchi wale waweze kunufaika na kilimo cha kisasa.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa Serikali imekuwa ikipanga miradi mingi ya umwagiliaji katika mkoa wa Morogoro ambayo haitekelezeki, je, Serikali sasa haioni kuna haja ya kwuaatumia wataalam ambao wanatoka Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA) waweze kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Morogoro kuendeleza kilimo cha umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wizarani pamoja na changamoto ambazo tumeziona tukaona haja sasa ya kupitia ule mpango kabambe, na tumejipanga katika kuhakikisha tunakuwa na miradi michache lakini yenye tija ya uzalishaji katika nchi yetu. Kwa hiyo, wazo lako na ushauri wako tumeupokea katika kuhakikisha tunaboresha miundombinu ya umwagiliaji ili iweze kuwa na tija katika nchi yetu.
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize maswali mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu mstaafu alipotembelea kwenye kijiji hiki alikuta tayari Serikali imeshaanza kutekeleza, lakini yalijitokeza mapungufu ambayo yalikuwa yanagharimu milioni 295,000,000 kwa ajili ya kujenga mifereji (main canal), kwa ajili ya kujenga vivuko vya watu na wanyama na kwa ajili ya kujenga vigawa maji kuelekea mashambani. Pia kumalizia na kuongeza eneo la mfereji lifike kilometa 2.2 na ndiyo maana Mheshimiwa Waziri Mkuu baada ya kuona hilo akaahidi kwa wale wananchi wa Nundwe kwamba niko tayari kutoa shilingi 295,000,000 mradi huu uweze kukamilika. Mradi huu ukikamilika utaajiri vijana…
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakwenda kwenye swali, utaajiri vijana walio wengi. Sasa swali langu hapa linasema lini hiyo shilingi 295,000,000 itatoka kusudi haya mambo ambayo tunayazungumza yaweze kutekelezwa Mheshimiwa Waziri? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nilikuwa namuomba sana Mheshimiwa Naibu Waziri au Waziri aje kwenye site aone hili jambo ambalo tunalizungumzia.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge mzee wangu Mgimwa, lakini pia nitumie nafasi hii kumpongeza kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. Kwa hiyo kama Mwenyekiti wangu ahadi ni deni na sisi kama viongozi wa Wizara hii hatutokuwa kikwazo katika kuhakikisha tunakamilisha ahadi ile ambayo imetolewa na Waziri Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Mizengo Pinda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu ahadi ya mimi kwenda kule katika jimbo lake, nipo tayari Mheshimiwa Mbunge na Mwenyekiti wangu kuongozana pamoja katika kuangalia hali halisi ya utekelezaji wa mradi ule ili hatimaye tuongeze jitihada kwa haraka. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza nimshukuru Waziri kwa utekelezaji wa mradi wa visima katika Jimbo la Nzega. Naomba kujua mwaka 2015 moja ya hadi kubwa ya Mheshimiwa Rais ilikuwa ni kufufua skimu ya umwagiliaji katika Kijiji cha Idudumo katika Halmashauri ya Mji wa Nzega. Je, ni lini ahadi hii Serikali itaanza utekelezaji wake kwa ajili ya kulipitia na kulirekebisha bwawa hilo na kutekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na napenda nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge juu ni lini utekelezaji. Miradi ya utekelezaji wa umwagiliaji inategemeana na fedha. Fedha zitakapopatikana ka wakati na sisi tutatekeleza kwa wakati katika kuhakikisha mradi huu unakamilika. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa matatizo ya Geita yanafanana kabisa na yale ya Wilaya ya Kigamboni na Mbagala katika Wilaya ya Temeke, pamoja na juhudi za Serikali za kuchimba visima virefu katika Kata ya Kisarawe II Wilaya ya Kigamboni, lakini wananchi wale hawana kabisa mtandao wa maji safi na salama.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuweka mtandao wa maji safi na salama katika Wilaya ya Kigamboni na maeneo ya Mbagala? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kumpongeza sana mama yangu, Mheshimiwa Mariam kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake, lakini kubwa mimi kama Naibu Waziri nilipata kibali cha kufanya ziara katika Mkoa wa Dar es Salaam na moja ya maeneo ambayo nilifanya ziara ni eneo la Kigamboni, Temeke na maeneo mengine. Ni kweli zipo changamoto katika suala zima la maji, hususan pembezoni mwa Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji tumechimba visima 20 pale Mpera na Kimbiji katika kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji, lakini visima vile bado havijafanyiwa utandazaji. Sisi kama Wizara tumeona haja sasa ya kufanya phase one ili kuhakikisha wananchi wale wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Kwa hiyo, Mheshimiwa mama yangu Mheshimiwa Mariam, sisi kama Wizara ya Maji na kwa kuwa siyo Wizara ya ukame, tupo tayari kuhakikisha wananchi wa Kigamboni wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la msingi lilisema ni lini Serikali itamalizia Skimu ya Ipatagwa, Kongoro/Mswiswi na Motombaya, itamalizia lini? Naomba Mheshimiwa Waziri aniambie Serikali itamalizia lini skimu hii ambayo ilishaanza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, matatizo ya wananchi wa Mbarali yanafanana sana na matatizo ya wananchi wa Chunya ambako kuna Bwawa kubwa la Matwiga ambalo linajengwa kwa msaada wa Serikali ambalo limefikia asilimia karibu 80. Je, Serikali ni lini itamalizia ujenzi wa bwawa hili?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sisi kama Wizara ya Maji tunatambua kabisa umuhimu wa umwagiliaJi na tunatambua asilimia kubwa ya wananchi wanaishi vijijini na kilimo wanachotegemea ni kilimo cha kudra za Mwenyezi Mungu kwa maana ya kwamba mpaka mvua inyeshe. Hata hivyo, kwa kuwa sasa hivi tunaenda katika Tanzania ya viwanda, tunatambua tunapoenda katika kilimo cha umwagiliaji tutaweza kuwa na kilimo cha kisasa na tutaweza kupata mazao ambayo yatakuwa toshelevu kwa chakula lakini hata katika viwanda vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kilimo cha umwagiliaji, sisi kama Wizara ya Maji tumeona kumekuwa na changamoto nyingi sana; moja, kumekuwa na miradi mingi lakini haijakamilika, tumekuwa na skimu za umwagiliaji lakini hakina chanzo cha maji, kinalima msimu mmoja. Waziri wangu ameona haja ya kupitia masterplan ya kilimo kile cha umwagiliaji ili tuwe na njia bora sasa, tuwe na miradi michache lakini itakuwa na tija kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupitia sasa, moja ya miradi ambayo Mheshimiwa Mbunge ameorodhesha Mbarali na eneo lake, tutatekeleza kwa wakati katika kuhakikisha tunakipa nguvu kilimo hiki cha umwagiliaji.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri. Mheshimiwa Waziri alikuja Mufindi na alikuja kwenye Kata ile ya Mtwango. Mradi wa Kata ya Mtwango una miaka karibu sita na mkandarasi yupo site, Serikali haijapeleka fedha mpaka leo. Hebu awaambie wananchi wa Kata ya Mtwango, ni lini Serikali itapeleka fedha kwenye kata ile?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, naishukuru Serikali kwa kutenga bilioni 2.67 kwa ajili ya Miradi ya Igowole, Mtambula, Nyololo, Idunda na Itandula. Sasa, je, Naibu Waziri, ni lini atakuja katika Jimbo la Mufindi Kusini awaeleze haya aliyoeleza leo Bungeni? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana kwa kazi kubwa anayoifanya na amekuwa na usumbufu mkubwa sana kuhusu suala zima la maji katika Jimbo lake. Naendelea kusema sisi Wizara ya Maji na kwa kuwa siyo Wizara ya Ukame, nataka nimwambie Katibu wangu Mkuu ndani ya mwezi huu tutapeleka fedha wananchi wako waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusu mimi kwenda Mufindi, nipo tayari, baada ya Bunge tuongozane na Mheshimiwa Mbunge twende tukazungumze na wananchi wake. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa natambua uwepo wa Simba hapa ndani, lakini pia niwaombe watoe tofauti zao na zetu ili waweze kuwaombea Yanga waweze kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu linasema hivi, kwa kuwa kuna skimu kubwa ya umwagiliaji kule Mahenge, Mgambilenga, je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kutembelea mradi ule kwa sababu ni muda mrefu sasa haujafanyiwa kazi kwa sababu fedha nyingi zilikuwa zinatoka nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nipo tayari na nadhani katika ziara nitakayokwenda Mufindi nitapita katika Jimbo la Mheshimiwa Mbunge. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa Ibofwe uko Mkoani Iringa ambao unahudumia vijiji 10. Nilikwishauliza swali la msingi nikajibiwa kwamba shilingi milioni 49 zitatolewa baada ya kutoka certificate. Certificate ilishatolewa pesa hazijapatikana toka mwaka jana, naomba kujua ni lini pesa hizo zitatolewa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitumie nafasi hii kumjibu Mheshimiwa Mbunge, kwa kuwa maji ni uhai na sisi kama Wizara ya Maji hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Iringa, namuomba Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge tukae na wataalam wetu tuangalie namna ya kuzipeleka fedha hizo wananchi wapate maji.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kunipa nafasi hii. Eneo la Mishamo ni eneo ambalo liliishi wakimbizi na sasa hivi ni Watanzania wapya ambao wamepewa uraia na Serikali. Eneo hili kupitia Shirika la UNHCR lilichimba visima karibu vijiji 16, vijiji hivyo kwa sasa havina maji kwani visima hivyo vilishaharibika. Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia kufufua visima hivyo ambavyo kimsingi vikifufuliwa na Serikali vitatatua kero ya maji katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake lakini kwa namna bora ya kuhakikisha wananchi wake wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara ya Maji tumekuwa na taratibu ya kufufua visima vyote ambavyo vimekufa kwa kuvirudisha katika hali yake ili wananchi waweze kupata maji. Nipo tayari kuongozana naye kwenda kuona hali halisi ili mwisho wa siku tupange namna gani tunaweza tukavifufua visima vile ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mradi wa Maji wa Kijiji cha Getamok, Namahaha na sasa Endonyoet katika Wilaya ya Karatu iliojengwa chini ya Mpango wa WSDP I haufanyi kazi kwa sababu ya kujengwa chini ya kiwango. Serikali ilituma wataalam wake kukagua tatizo hilo ili kubaini kiwango ambacho kingehitajika kufufua miradi hiyo. Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha ili kurudisha huduma hiyo muhimu kwa wananchi?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Qambalo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tumeunda Tume maalum ya wataalam watakaohusisha sekta mbalimbali za Serikali. Tutachukua pamoja na hiyo ripoti ambayo anasema kwamba Serikali ilituma timu tuiangalie ili tukishabaini sasa ule upungufu tutatoa fedha na kukarabati mradi husika.
MHE. OMARI A. KIGODA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya maji Handeni na Kilindi ipo kwa muda mrefu sana na sababu kubwa nyingi ni miradi ambayo imefanywa chini ya kiwango. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari baada ya Bunge twende wote tukakague miradi ile na Serikali iweze kuwatolea maamuzi kwa wahusika wote walioshiriki katika kutekeleza miradi hiyo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge Omari Kigua na kaka yangu Mheshimiwa Kigoda kwa namna ya kipekee wa ufuatiliaji wao wa maendeleo ya majimbo yao kwa wananchi wa Handeni pamoja na Kilindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa Serikali imekuwa ikitoa fedha nyingi sana kutekeleza miradi ya maji lakini wapo baadhi ya wajanja wajanja kwa maana ya wakandarasi na wahandisi wanahujumu fedha hizi za Serikali. Huruma hailei mwana. Sisi kama viongozi wa Wizara hatutomuonea haya mtu yeyote. Yapo maneno yanayosema kwamba eti huyu ni mtu wa kigogo tutamuonea haya, hata awe mtoto wa kigogo cha namna gani tutatumia chainsaw kulicharanga awe kuni wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya Wizara ya Maji ya mwaka 2016/2017 uliwekwa mpango wa kujenga bwawa la umwagiliaji la Bonde la Mto Ruhuhu ambalo linahusisha Wilaya ya Nyasa na Wilaya ya Ludewa. Je, mpango ule umefikia wapi kwa sababu kwenye bajeti ya mwaka huu hatujauona?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge lakini kikubwa tunatambua kabisa kilimo cha umwagiliaji ndiyo kitakachotoa Watanzania na kufikia azma ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa sisi kama Wizara tumeona kumekuwa na changamoto kubwa sana katika miradi ya umwagiliaji. Moja, miradi imekuwa mingi lakini haijakamilika na hata iliyokamilika imekuwa ikilima msimu mmoja tu kwa sababu hakuna chanzo cha maji. Kwa hiyo, tunapozungumzia umwagiliaji maana yake ni kilimo mbadala. Wizara kwa kupitia wahisani wetu wameona haja sasa ya kupitia miradi yote ya umwagiliaji ili tuwe na mpango mahsusi utakaoweza kusaidia miradi michache lakini itakayokuwa na tija katika kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wananufaika na kilimo cha umwagiliaji. Baada ya mapitio hayo na katika eneo la Jimbo la Ludewa tutaangalia namna ya kuweza kusaidia jimbo hilo. Ahsante sana.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tatizo kama hili la maji ya mvua ambayo yanapotea siyo tu kwamba liko huku Kilindi lakini hata kule kwetu Meru na siyo kupotea peke yake bali pia kusababisha maafa. Miaka ya 80 mwanzoni wakati Waziri Mkuu akiwa Marehemu Sokoine yalitokea maafa makubwa sana yaliyosababishwa na maji kwenye ukanda wa chini wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru. Iliundwa timu wakati ule ...

Mheshimiwa Mwenyekiti, najenga hoja tu ili waone umuhimu wa suala lenyewe tafadhali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba mwaka 2009, Ofisi ya Waziri Mkuu ilikuja Meru na walitengeneza dossier kubwa sana ambayo ilitoa mapendekezo ya kukinga maji ili yatumike kwa kilimo cha umwagiliaji kwenye Kata za Mbuguni, Shambaraiburuka pamoja na Makiba. Mapendekezo hayo hayakufanyiwa kazi na mwaka huu wananchi wana maafa makubwa. Hivi tunavyoongea sasa hivi wameshindwa kutembea mpaka Wizara ya Afya imepeleka Mobile Services kwa ajili ya kusaidia watu wa eneo lile. Namuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba ni lini watatumia ile ripoti ili kuweza kukinga maji na kuokoa watu wa Kata za Mbuguni, Shambaraiburuka na Makiba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze sana kaka yangu Mheshimiwa Nassari kwa namna anavyowatetea wananchi wake lakini kubwa sisi tumepokea hayo aliyoyaeleza. Mimi kama Naibu Waziri tutakaa na wataalam wetu tuyapitie mapendekezo hayo tujue namna ya kufanya. Ahsante sana.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali, kwanza mradi wa Sepeko Lendikinya mwisho wake kwa mujibu wa mkataba ni Juni 2018. Kwa hiyo, ni muhimu Wizara ikachukua hatua ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize sasa maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, tatizo la maji katika Shule hii ya Nanja Sekondari limekuwa la muda mrefu na kusababisha adha ya wanafunzi kuacha masomo na kwenda kutafuta maji katika malambo upande wa pili wa barabara ambao ni hatari kwa usalama wao. Je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba fedha hizi ambazo Wizara imetenga mwaka huu na mpaka sasa haujaanza zinapelekwa ili mradi huu uweze kukamilika kwa haraka na wanafunzi wale waweze kupata maji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mradi huu wa mabwawa ni wa muda mrefu na utagharimu fedha nyingi shilingi bilioni 1.4, ni kwa nini sasa Serikali kupitia DDCA isichimbe visima vifupi katika Kata ya Makuyuni Esilalei ambako ni gharama nafuu na kwa haraka zaidi ili wananchi hao waondokane na adha ya maji ambayo imechukua muda mrefu sasa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua changamoto kubwa ya maji baadhi ya maeneo mbalimbali, Serikali imekuwa ikitenga fedha katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji. Nimwombe Mhandisi wa Maji wa Monduli asilale, Serikali imeshatenga fedha, ahakikishe ana-raise certificate ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza pamoja na wanafunzi wa shule hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kubwa ni kuhusu suala la uchimbaji visima DDCA. Nimuombe tu Mhandisi wa Maji aingie mkataba na watu wa DDCA na ile fedha aliyopangiwa ili watu wa DDCA waanze kazi ile mara moja. Ahsante sana.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyoelezwa kwenye swali la msingi kwamba wananchi 803 wa Kata za Matogoro na Seedfarm wanadai fidia ya kiasi cha shilingi bilioni 1.9, lakini majibu ya Serikali wamesema katika mwaka wa fedha 2017/2018 watalipa, mimi nafahamu mwaka wa fedha 2017/2018 unaishia hivi karibuni watalipa milioni 500. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kiasi hiki kilichobaki kinalipwa kwa wakati?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa malipo haya yamechelewa; Je Serikali haioni kwamba iko haja ya kuwalipa wananchi hawa pamoja na fidia kwa kuwa jambo hili limekuwa la muda mrefu? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WA WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nitumie nafasi kumpongeza dada yangu Sikudhani Chikambo pamoja na Mheshimiwa Mbunge wa Songea Mjini kwa namna wanavo wapigania wananchi wa Majimbo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji kwa kuona wananchi wale wametoa eneo kwa ajili ya chanzo cha maji, Wizara yetu ikaona haja ya kulipa. Nadhani kabla ya bajeti hii kuisha tutawalipa fedha zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kiasi kilichobakia nitumie nafasi hii kwanza kulipongeza Bunge lako Tukufu kwa kutuidhinishia Bajeti yetu ya Maji na katika fedha zile kiasi ambacho kilibakia tumeshawatengea fedha wananchi wa Songea. Kikubwa nimwombe Mheshimiwa Mbunge akawasimamie wananchi wake waende kuzitumia fedha zile vizuri, badala ya kwenda kuongeza familia nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji na Umwagiliaji hatuko kwa ajili ya kuwadhulumu, kikubwa fedha hizi zitatoka kwa wakati katika kuhakikisha tunawalipa fidia wananchi wake. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DUA W. NKURUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Mheshimiwa Akbar amekuwa akiliuliza swali hili mara kwa mara, je, Mheshimiwa Waziri haoni umuhimu wa kutembelea Jimbo lake ili aweze kujionea hali halisi ya kule?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Vijiji vya Masuguru, Mtambaswala, Nanderu, Ngonji na Marumba vimepitiwa na Bonde hili la Mto Ruvuma katika Jimbo la Nanyumbu, je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapatia wananchi hawa skimu ya umwagiliaji ili kuwakwamua katika hali ya maisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Akbar kwa namna anavyowatetea wananchi wake. Ni kweli amekuwa akiliuliza swali hili na amekuwa akilifuatilia mara kwa mara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya jukumu la Naibu Waziri ni kufuatilia miradi na kwenda kuangalia uhalisia. Niko tayari kwenda kuona mradi huo kama alivyoomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mkakati wa kilimo cha umwagiliaji Nanyumbu, sisi kama Wizara ya Maji tuna eneo la hekta milioni 29.4 linalofaa kwa kilimo cha umwagiliaji na katika mikakati yetu ambayo tunataka kuhakikisha kwamba umwagiliaji unakuwa na tija kubwa kwenye uzalishaji, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Nanyumbu, hatutawasahau wala hatutawaacha wananchi wa Nanyumbu katika kuhakikisha tunawapa kilimo cha umwagiliaji. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nami niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kushirikiana na Mbunge mwenzangu wa Bahi, Mheshimiwa Badwel, tumeweza kuchonga mfereji kutoka Mto Bubu kwenda kwenye vijiji vyetu kwenye skimu za umwagiliaji kwa kushirikiana na wananchi na Mfuko wangu wa Jimbo. Je, Serikali itakuwa tayari kutusaidia kuboresha miundombinu kwa maana ya mifereji midogo pamoja na mabanio katika Vijiji vyangu vya Lusilule, Udimaa, Ndamloi na Igose?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mtuka pamoja na Mheshimiwa Badwel wa Bahi kwa mapenzi ya dhati kwa wananchi wao katika kuhakikisha wanawasaidia. Sisi kama Wizara ya Maji katika kuwaunga mkono, hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha tunawasaidia ili wananchi wao waweze kupata miundombinu mizuri.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtemi, nakushukuru kwa kunipa fursa hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Lindi, tuna mto ambao una-flow maji kipindi chote, Mto Lukuledi unaopatikana katika Jimbo la Mtama na kuna skimu za umwagiliaji ambazo zilianzishwa na Serikali lakini kwa bahati mbaya zimeishia katikati, zime-stuck sasa zaidi ya miaka mitano. Tunataka kujua ni lini Serikali itakwenda kufanya upembuzi ili kujua kitu gani kilikwamisha na kuweza kufanya mpango ili zile skimu ziweze kufanya kazi yake kama ilivyokuwa imekusudiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge. La pili, tuna skimu zaidi ya 2,947. Sisi kama Wizara kwa muda huu tumeona tuna skimu nyingi lakini kwenye uzalishaji matokeo ni madogo sana. Waziri wangu akaona haja ya kuunda timu kuangalia changamoto zilizoko katika hizi skimu za umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto tulizoziona, tuna skimu nyingi lakini bado hazijakamilika. Mkakati wetu ni kwamba tunataka tuwe na skimu chache lakini ziwe na tija kubwa ili tuweze kufikia uchumi wetu ule wa viwanda katika kuhakikisha tunakuwa na kilimo cha umwagiliaji kizuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri na kwamba kweli ujenzi wa matenki unaendelea, lakini kuna maeneo mengine ambayo ni korofi kama Mabwepande, Kijiji cha Mbopo na maeneo mbalimbali ya Kata ya Mbezi ikiwemo Mtaa wa Ndumbwanji. Ni lini sasa Serikali itatia mkazo kuhakikisha maeneo hayo yanapatiwa maji kwa haraka sana kwa sababu kumekuwa na shida?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Manispaa ya Iringa na Iringa kwa ujumla inategemewa kuwa ni kitovu kikubwa cha utalii wa Kusini na Manispaa ya Iringa imebakiza asilimia nne za upatikanaji wa maji. Je, ni lini sasa hizo asilimia nne zitaisha ili watalii watakapofika kule wasipate matatizo wanapokwenda katika maeneo yale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya jitihada kubwa sana kuondoa tatizo la maji katika Mkoa wa Dar es Salaam na mpaka sasa hali ya upatikanaji ipo katika asilimia 75 lakini yapo maeneo ambayo hayana maji. Serikali kwa kuona hilo sasa kuna mradi ambao unatekelezwa kutoka Mpiji – Tegeta
(a) Bagamoyo lakini Mbezi mpaka kwa kaka yangu Mheshimiwa Mnyika katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji.
Kwa hiyo, mpaka mkataba huu utakapokuwa umesainiwa na kupata kibali kutoka Benki ya Dunia tutatekeleza kwa wakati ili wananchi wa Dar es Salaam waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kulishukuru Bunge lako Tukufu, katika bajeti yetu ya Wizara ya Maji tumepitishiwa kiasi cha shilingi 727,345,000,000. Katika fedha hizo tutauangalia Mji wa Iringa katika kuhakikisha tunaondoa tatizo la maji. Ahsante sana.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba sasa nimuulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, tatizo kubwa hapa ni uhaba wa wataalam. Naomba kujua sasa Serikali itatupatia lini wataalam wa kuweza kutusaidia katika kurahisisha ukamilishaji wa hii miradi ya maji inayoendelea huko Mbogwe? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, naomba sasa kujua time frame, ni lini miradi hii itakamilishwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyowatetea wananchi wake lakini kikubwa maji hayana mbadala na uhitaji wa maji ni mkubwa sana. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo, kubwa nimwombe Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane ili tuwape watalaam wetu wa Wizara waweze kumsaidia katika kuhakikisha wananchi wake wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuhusu suala zima la fedha na ni lini miradi hii itakamilika, kikubwa nimwombe sasa Mhandisi wa Maji katika Jimbo lake ahakikishe kwamba anatengeneza certificate ili sisi kama Wizara tutawalipa kwa wakati ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kondoa Mjini tulichimba visima kumi, tumepata usambazaji wa visima vitano, lakini bila ya ukarabati wa miundombinu ya maji pale mjini, hizi gharama zilizotumika kusambaza visima vitano ni sawa na bure.
Je, ni lini Serikali itatuletea fedha kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya maji mjini ambayo pia ni ahadi ya Waziri Mkuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, nikushukuru lakini kikubwa nataka nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Sannda kwa jitihada anazozifanya, sisi kama Wizara ya Maji lazima tumuunge mkono. Kikubwa nimuombe Mhandisi wa Halmashauri ya Kondoa asilale, fedha tumeshapitishiwa na Bunge a-rise certificate na sisi tutamlipa kwa wakati mkandarasi atakayetekeleza mradi huo katika kuhakikisha tunaondoa tatizo la maji.
MHE. SILAFU J. MAUFI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili madogo ya kuiuliza Serikali yangu.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, mikoa hii ya pembezoni Serikali imekuwa inasuasua kuwapelekea huduma zinazohitajika kwa maendeleo ya jamii. Napenda kuiambia Serikali kwamba huu uzoefu walioupata kutoka Ziwa Victoria kupeleka maji Shinyanga, Tabora, Simiyu na kadhalika naomba basi uzoefu huu wakaupeleke katika mikoa ya Katavi, Rukwa na Kigoma. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hii speed ya kupeleka maji katika Mji wa Ujiji ni ndogo sana, haina matunda mazuri kwa mikoa hii mitatu. Je, Serikali inasema nini katika kuhamisha uzoefu huu wa Ziwa Victoria na kuuweka katika mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali haioni kwamba inatumia fedha nyingi za kuchimba visima virefu katika vyanzo ambavyo havina uhakika, inaonaje ikatumia vyanzo hivi ambavyo ni vya uhakika…
Mheshimiwa Spika, ni katika kujenga hoja na kuweka mambo sawa. Napenda kufahamu ni lini hii awamu ya pili itaanza ili hivi vyanzo vya uhakika vya Ziwa Tanganyika na Ziwa Rukwa vifanyiwa kazi ili wananchi wa Rukwa wapate maji ya uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge na ukimuona mtu mzima analia ujue kuna jambo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, najua changamoto kubwa sana ya maji katika eneo lake. Sisi kama Wizara tupo tayari sasa kutoa ushirikiano na uzoefu wetu katika kuhakikisha wananchi wake wa maeneo ya Rukwa wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Spika, ikumbukwe sisi ni Wizara ya Maji na siyo Wizara ya Ukame, tupo tayari kuwapatia maji wananchi wa Rukwa.
Mheshimiwa Spika, katika kuongeza jitihada, nipo tayari kufanya ziara maeneo ya Mheshimiwa Mbunge ili kuangalia namna ya kuweza kutatua tatizo hili kwa haraka. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Spika, changamoto ya tatizo la maji safi na salama kwa wananchi wa Manispaa ya Morogoro bado ni kizungumkuti. Bwawa la Mindu ambalo limekuwa likitegemewa na wananchi wa Manispaa kwa sasa halitoshelezi. Kwa kuwa Mkoa wa Morogoro una mito mingi, je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga bwawa lingine ili iwe mwarobaini kwa wananchi wa Manispaa ya Morogoro ambao wanakosa maji kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge dada yangu Devotha, ni kweli Morogoro kumekuwa na changamoto kubwa sana ya maji na tunajua kabisa tunaelekea Tanzania ya Viwanda, lazima tuwe na mahitaji ya maji kwa maana ya maji yenye utoshelevu. Sisi kama Wizara ya Maji tumeliona hilo, tupo kwenye majadiliano ya dola milioni 70 katika kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo la maji safi na salama katika Mkoa wa Morogoro. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba niiulize Serikali ni lini itapeleka maji kwenye Kata ya Mjele ambayo ni ahadi ya muda mrefu ya Serikali? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitumie nafasi hii nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya na nimeshafika hadi Mjele. Namwomba sana Mhandisi wa Maji wa Jimbo la Mbeya Vijijini asilale ili kuhakikisha wananchi wale wanapata maji safi, salama na ya kuwatosheleza. Jambo la msingi sisi kama Wizara a-raise certificate tuko tayari kulipa kwa wakati ili wananchi waweze kupata maji.
MHE. IGNAS A. MALOCHA. Mheshimiwa Naibu Spika ahsante sana. Kwanza nimpongeze Naibu Waziri na Waziri wake kwa utendaji wa kazi, lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, mradi huu wa Muze Group unategemewa kupeleka maji katika vijiji 10 vyenye wakazi 40,000 ambavyo ni Kijiji cha Kalumbaleza A, B, Muze, Mbwilo, Mlia, Mnazi mmoja Asilia, Ilanga Kalakala, Izia na Isangwa. Maeneo haya hukumbwa na kipindupindu kila mwaka kutokanana na shida ya maji, mwaka huu wananchi wapatao 605 waliugua kipindupindu, katika hao wananchi 15 walikufa. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuharakisha ujenzi wa mradi huu ili kunusuru vifo kwa wananchi?
Swali la pili, kwa vile Mtaalam Mshauri wa mradi huu alishaanza kazi na amesha- raise certificate Wizara ya Maji; Je, ni lini watamlipa fedha zake haraka ili mradi huu uweze kuanza mapema? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna ya kipekee anavyowatetea wananchi wake. Nataka niwahakikishie kwamba maji ni uhai, Wizara ya Maji hatutakuwa sehemu ya kupoteza uhai wa wananchi wake. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutakuwa sehemu ya kusimamia mradi huu ili uweze kutekelezeka kwa wakati wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya Bunge cha saa saba tukutane ili twende kuhakikisha Mkandarasi huyu analipwa kwa wakati ili mradi usikwame na wananchi waweze kupata maji. (Makofi)
MHE. HALIMA ABDALLAH BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Moja ya changamoto mbalimbali za maji ni ukosefu wa vyanzo vya maji, lakini sisi Mkoa wa Kagera Mwenyezi Mungu ametujaalia tuna vyanzo vingi vya maji. Ukiachilia mbali Ziwa Victoria tuna mito mingi ukiwemo Mto Kagera, lakini shida ya maji imekuwa ni kubwa zaidi na kuna wakati Wilaya ya Ngara kuna wanafunzi walilipotiwa kukosa masomo kwa sababu ya kutafuta maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo Serikali imekuwa ikitekeleza miradi mikubwa ya maji nchini lakini Mkoa wa Kagera umekuwa ukiwekwa pembeni. Waziri atakubaliana na mimi sasa umefika muda Mkoa wa Kagera uwe una mradi mkubwa mmoja wa maji ili uweze kusambaza maji katika vijiji vyote vya Mkoa wa Kagera na huyo Mkandarasi Mshauri atakubali suala hili la kimkakati?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu langu la pili, Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika la AFD lilikubali kufadhili Mradi wa Maji Bukoba Mjini. Je, Serikali ipo tayari kuwaomba Serikali ya Ufaransa iendelee kufadhili Mkoa wa Kagera ili waweze kutatua tatizo la maji kuwasaidia wananchi hasa hasa akinamama na watoto wa Mkoa wa Kagera? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILAIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekati, napenda kumpongeza mdogo wangu Mheshimiwa Halima Bulembo; ni miongoni mwa Wabunge makini sana katika Bunge hili na amekuwa ni mtetezi mkubwa sana kwa akinamama na watoto katika suala zima la maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie, jukumu la Wizara ya Maji ni kuhakikisha Wanakagera wanapata maji na si maji tu, ni kwa maana ya maji safi salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu kwa kuona hali ya changamoto ya maji kwa Mkoa wa Kagera tumetekeleza Mradi mkubwa sana katika Mji wa Kagera zaidi ya bilioni thelathini na mbili katika kuhakikisha wananchi wa Bukoba wanapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; tuna mradi mwingine katika miji 17, tunaenda kujenga mradi mkubwa sana katika Mji wa Kayanga kwa kaka yangu Mheshimiwa Bashungwa katika kuhakikisha wananchi wa Kagera wanaenda kupata maji hayo. Kingine, katika Bajeti ya mwaka 2018/ 2019 tumetenga zaidi ya Sh.13,520,000,000/= katika kuhakikisha wananchi wa Kagera wanapata maji. Niwaombe sana wataalam wetu wa maji wa Mkoa wa Kagera wasilale na Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Kagera wasimamie fedha hizi katika kuhakikisha zinaenda kutatua tatizo la maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili nataka nimtie moyo Mheshimiwa Mbunge; ukisoma Mathayo-7 inasema ombeni nanyi mtapewa, bisheni hodi nanyi mtafunguliwa. Tumeshawafungulia wananchi wa Kagera, sisi tuko tayari kuendelea kuwatafuta wafadhili katika kuhakikisha tunaenda kutatua tatizo la maji Kagera. Ahsante sana. (Makofi)
MHE.RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii mito inapeleka mpaka Mbuga ya Katavi lakini kwa mujibu wa sheria watu wote wana haki. Sasa niombe ni lini sasa Serikali itakamilisha kandarasi hiyo upembuzi yakinifu ili katika bajeti ya mwaka 2019/2020 tuweze kutengewa fedha kwa ajili ya skimu ya umwagiliaji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna mradi wa umwagiliaji uliopo kwenye kata ya Ugala ambapo una miaka mingi haujakamilika na mifereji bado na unasimamia na Mamlaka ya Bonde makao makuu yaliyoko Mbeya. Sasa Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha ili kukamilisha mradi huu ili uweze kutumika na wananchi katika uzalishaji na kuinua maeneo yao ya kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri na namna anavyofuatilia changamoto za wananchi wake. Kubwa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji kutokana na changamoto hiyo katika umwagiliaji, tumeona haja sasa ya kufanya upembuzi wa haraka. Kubwa ambalo nataka nimhakikishie, tutafanya usimamizi wa haraka ili mwisho wa siku hili jambo liweze kukamilika na ujenzi ule uweze ujengwa kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la ukamilishaji wa mradi aliouelezea, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama Wizara yetu ya Maji tumeainisha miradi ambayo haijakamilika. Tumeona tumekuwa na miradi zaidi ya 1,967 ambayo haijakamilika. Kwa hiyo, wajibu wetu ni kuhakikisha tunaikamilisha ili mwisho wa siku iwe na mchango mkubwa sana katika uchumi wetu wa kati. Tunajua kabisa umwagiliaji ni kilimo cha mbadala ambacho kina mchango mkubwa kabisa katika suala zima la uchumi kwa maana ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutalisimamia hili jambo mradi wao ukamilike ili uweze kuwa na tija kwa wananchi wake. (Makofi)
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mradi wa Umwagiliaji wa Mwamkulu ni takribani miaka nane sasa haujakamilika na wananchi wa eneo hilo walivunjiwa vizibo. Napenda kuiuliza Serikali, ni lini itapeleka fedha ili kuhakikisha mradi huo umekamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri. Nimhakikishie kwamba hili jambo ni la haraka. Kwa hiyo, sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga katika kuhakikisha tunalikamilisha hili jambo ili wananchi wake waweze kunufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Mbunge pia baada ya saa saba mchana tunaweza tukakutana tujadiliane kwa pamoja ili tuone ni namna gani tunaweza tukalifanya hili jambo ili liweze kukamilka kwa wakati.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Njombe ni Mji unaokuwa kwa kasi sana na upo katika Miji 17 ambayo imeahidiwa kutengenezewa miradi mikubwa ya maji na Mji wa Njombe unategemea kupata maji kutoka Mto wa Gafilo.
Je, ni lini huu mradi sasa utaanza ili kusudi wananchi wa Njombe waweze kupata maji safi na salama?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji na tunatambua kabisa katika Mkoa wa Njombe ni moja ya Mikoa ambayo ina changamoto kubwa sana katika suala zima la maji. Wizara yetu ina miradi zaidi ya 17 kwa maana ya mkopo nafuu katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo lolote kubwa ambalo lina mafanikio makubwa, lazima linakuwa na taratibu zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuko katika taratibu za manunuzi. Pindi manunuzi yatakapokuwa yamekamilika, tutampata Mkandarasi katika kuhakikisha mradi ule unakamilika kwa wakati kwa wananchi wake wa Njombe. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupongeza kwa kuendesha vizuri Bunge letu na ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Hanang ni moja ya Wilaya ambazo mvua hazina uhakika na ninaishukuru Serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya mradi wa Endagau wa umwagiliaji. Hata hivyo, mradi huo ulikuwa na mushkeli. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kama wametoa fedha za kutosha kusahihisha yale mambo ya kitaaluma ambayo hayakwenda vizuri na umwagiliaji hauendi vizuri ili wananchi wa Hanang waweze kuwa na uhakika wa kupata chakula kutokana na umwagiliaji.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu imekuwa inafanya jitihada kubwa sana ya kutoa fedha katika kuhakikisha inakamilisha miradi mbalimbali. Itakuwa ni jambo la aibu na fedheha kwamba tunapeleka fedha halafu hazifanyi kazi kama ilivyotarajiwa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge tutafika hapo katika Jimbo lake ili kuweza kuhakikisha kama fedha zimepelekwa, nao kwa nini wasizitumie kama ilivyotarajiwa? Kama kuna ubadhirifu wowote, tutaweza kuchukua hatua kwa wale wahusika.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunikumbuka ingawa ulitaka tena unifute.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwulize Waziri wa Maji kwamba Jimbo la Same Mashariki lina mito mingi ambayo inatumika kwa umwagiliaji wa mpunga na tangawizi, lakini maji hayo yanapungua kila kuitwapo leo.
Je, Wizara ina mkakati gani wa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira ili wapate fedha ya kusaidia kutunza vyanzo vya maji ya mito hii mikubwa iliyoko katika Jimbo la Same Mashariki? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli na napenda kukubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba tumekuwa na vyanzo vingi sana katika nchi yetu, lakini kiukweli ukipita maeneo mbalimbali kuna baadhi ya vyanzo vimekauka, vingine vimefikia hatua hata kupotea, ni kwa sababu tu moja, ni mabadiliko ya tabia nchi, lakini pili, shughuli za kibinadamu, watu kulima karibu na vyanzo vya maji, wengine kufanya suala zima la ufugaji na wakati mwingine hata shughuli za uchimbaji madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu ya Maji tuna mabonde, kazi yao kubwa sana ni kusimamia rasilimali za maji ili ziweze kuwa endelevu. Kingine tunapokea ushauri kuweza kushirikiana na wenzetu hawa wa mazingira katika kuhakikisha tunavilinda na kuvitunza vyanzo vya maji viwe na faida ya sasa na vizazi vijavyo. Ahsante sana.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo ya nyongeza, lakini kabla sijauliza nilikuwa naomba nisahihishe jina langu, naitwa Ritta Enespher Kabati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri na mpango wao kabambe wa umwagiliaji, naomba nimwulize maswali mawili.
Kwa kuwa mradi huu wa Mkoga umekuwa ni mradi wa muda mrefu sana toka umeanzishwa katika Manispaa yetu. Tulikuwa tunategemea kama mradi huu ungekamilika, ungeweza kunufaisha zaidi ya wananchi 400 wakiwemo akina mama na vijana kuweza kujiajiri katika kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anihakikishie katika mwaka wa fedha 2019/2020 kama Serikali itaweza kutoa pesa ili kuweza kuukamilisha huu mradi ambao umekuwa wa muda mrefu sana? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, nilikuwa nataka kuuliza kwamba kwa kuwa katika Manispaa yetu hii ya Iringa bado tunao mradi mwingine wa Kitwiri Irrigation mradi ambao pia toka umeanzishwa haujawahi kupatiwa fedha, je, ni lini utapatiwa fedha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile namwomba Mheshimiwa Waziri kama yuko tayari kuja sasa katika mkoa wetu wa Iringa ili aitembelee hii miradi yote miwili na vilevile atembelee hata miradi mingine ya mkoa wetu wa Iringa ili iweze kukamilika na iweze kunufaisha wananchi wa mkoa wetu wa Iringa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, mama yangu Mheshimiwa Ritta Kabati, ni mmoja ya wamama shupavu sana katika kuhakikisha wanatetea matatizo ya wananchi wao katika Mkoa wa Iringa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati ya moyo wangu, tumekuwa na miradi mingi sana katika umwagiliaji zaidi ya 2000 lakini ni miradi 960 tu ndiyo iliyoendelezwa, zaidi ya miradi 1,967 haijaendelezwa. Sisi kama Wizara ya Maji, tukitambua kabisa umwagiliaji ndiyo kilimo mbadala ambao kinaweza kuchangia uchumi wa nchi yetu, tumeona haja sasa ya kuunda Tume ambayo itapitia mpango kabambe wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili tuwe na miradi michache ambayo itakuwa na tija kubwa sana katika nchi yetu kwa sababu tumekuwa na miradi mingine haina hata chanzo cha maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia suala la umwagiliaji, maana yake ni kilimo cha mbadala. Tunajua kabisa nchi yetu wakulima wengi wanalima kwa kutegemea kudra za Mwenyezi Mungu mpaka mvua inyeshe. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie, katika mpango huu kabambe tutakaoupitia katika mradi huu wa Mkoga, tutaupa kipaumbele katika kuhakikisha tunaukamilisha ili wananchi wake wa Iringa waweze kunufaika na kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kuhusu mimi kwenda Iringa, nataka nimwambie mwenda kwao haogopi kiza. Nitakwenda Iringa katika kuhakikisha naenda kuzungumza na wananchi wa Iringa ahsante sana. (Makofi)
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize swali moja la nyongeza.
Kwa kuwa Kata Ruaha Mbuyuni iko Kilolo - Iringa, Mheshimiwa Waziri Mkuu aliwahi kupita pale na kutoa ahadi, lakini baadaye Waziri husika alifika mwaka 2017 tarehe 28 Desemba akatoa ahadi kwamba Halmashauri ifanye designing na ipeleke mradi ule Wizarani ili yeye atoe kibali cha kutangaza. Sasa hivi imeshachukua muda mrefu na wananchi wanaendelea kusubiri.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri naye anasemaje ili wananchi wa Ruaha Mbuyuni waweze kupata uhakika kwamba sasa watapata maji safi na salama ili kipindupindu ambacho kimekuwa kikiwaua kwa muda mrefu kiache kuwaua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua maji ni huduma muhimu sana kwa wananchi na kwa kuwa hiyo ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, sisi tunatambua kabisa ahadi ni deni. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi hiyo tutaietekeleza ili kuhakikisha wananchi wake wanapata maji safi salama na yenye kutosheleza.
MHE. DANIEL N. NSWAZUNGWAKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi nina swali dogo la nyongeza kwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Scheme ya Umwagiliaji ya Msambala katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu ni scheme ambayo imetelekezwa, ina chanzo cha uhakika cha maji, lakini haipati fedha. Napenda kujua toka kwenye Wizara, ni kwa nini mradi huu muhimu umetelekezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Nia yetu sisi kama Serikali hatuna haja ya kutelekeza miradi, ila tumeona haja sasa ya kuunda Tume kubaini miradi ambayo itakuwa na tija kwa nchi yetu katika kuhakikisha tunaipelekea fedha ili iweze kuwa na tija kwa wananchi. Ahsante sana.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bwawa la Suke lililopo katika Kijiji cha Msange lilifanyiwa upembuzi tangu mwaka 2010 kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji kwenye Kata ya Msange, Makhojoa, Mwasawila na nyingine. Bwawa hili lilihitaji shilingi 1,300,000,000 na tangu mwaka 2010 hatujatengewa fedha mpaka sasa.
Je, ni lini tutapata fedha hizo kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa bwawa hilo ili wananchi waache kutegemea kilimo cha mvua? (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimwona mtu mzima analia, ujue kuna jambo. Naona Mheshimiwa Mbunge amelia sana kuhusu wananchi wake. Nataka niwahakikishie tutaona haja basi katika bajeti ya mwaka 2019/2020 ili tuangalie namna gani tunaweza tukasaidia hili jambo ili wananchi wake waweze kunufaika na mradi huu.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini iko miradi mingi ya maji ya umwagiliaji katika Mkoa wangu wa Ruvuma ambayo haijakamilika ikiwemo miradi ambayo iko katika Vijiji vya Legeza Mwendo, Misiaje na Kitanda Wilayani Tunduru. Miradi hii ilitakiwa ikamilike kupitia mpango wa ASDP Awamu ya Kwanza, lakini mpaka leo haijakamilika kwa ukosefu wa fedha.
Je, ni nini kauli ya Serikali katika kuhakikisha tunapeleka fedha za kukamilisha miradi hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze mama yangu Mheshimiwa Chikambo kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini kikubwa kama nilivyoeleza tumekuwa na miradi mingi ambayo haijakamalika, nasi kama Serikali tumeona haja ya haraka ya kuunda Tume.
Namwomba sana Mheshimiwa Mbunge, subira yavuta heri. Heri itapatikana pindi Tume itakapotuleta majibu ya haraka nasi tutaweza tukakamilisha. Ahsante sana.
MHE. YOSEPHER F. KOMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao mradi wa umwagiliaji katika Kata ya Misozwe, Jimbo la Muheza ambao umekamilika zaidi ya miaka kumi, lakini mradi ule mpaka sasa hivi haujaanza kwa sababu wananchi wa eneo lile ambalo lina mradi hawajalipwa fidia. Je, ni lini watalipwa fidia ili waweze kupisha mradi uanze?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali kuwa na nia ya utekeleza wa miradi mikubwa kwa ajili ya manufaa kwa wananchi, lakini zipo athari kwenye utekelezaji wa miradi kupita maeneo ya watu. Nataka niwahakikishie wananchi hawa, sisi kama Wizara ya Maji na Umwagiliaji tutahakikisha kwamba wale wananchi wanaostahili kulipwa wanalipwa fidia. Ila tutamlipa mwananchi anayestahili kulipwa na yule asiyestahili hatalipwa. Ahsante sana.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa iliingia mkataba na wenzetu wa DDCA kwa ajili ya kuchimba visima virefu toka mwaka 2017, lakini mpaka sasa mradi huu haujatekelezwa. Ni lini DDCA watatekeleza mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, lakini kubwa nampongeza Mheshimiwa Mbunge, Wizara yetu ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji. Sisi Wizara ya Maji siyo Wizara ya ukame nawaagiza ndugu zangu wa DCAA kuhakikisha miradi hiyo wanachimba kwa haraka ili wananchi wako wapate maji safi salama na yenye kutosheleza.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napenda kujua, pale katika scheme yetu ya umwagiliaji ya Choma Chankola tuna scheme ya umwagiliaji na Mheshimiwa Waziri alishawahi kuja kuona lile eneo na akaahidi tupeleke andiko kwa ajili ya uchimbaji wa bwawa kubwa pale. Tayari andiko limeshapelekwa katika Tume ya Taifa ya Umwagiliaji. Sasa ni lini fedha zitaweza kutolewa kwa ajili ya uchimbwaji wa bwawa hilo kwa sababu tayari ishapita miaka mitatu?Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza kaka yangu, Mheshimiwa Gulamali kwa namna anavyowatetea wananchi wake, lakini kubwa nataka nimhakikishie kwamba nami naomba nipitie hilo andiko kwa haraka ili mwisho wa siku tupate kushauriana na Mheshimwia Waziri wangu mpya, Mheshimiwa Mbarawa katika kuhakikisha hili jambo tunalikamilisha kama ilivyopangwa. (Makofi)
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kutokana na mabadiliko ya tabianchi, mashamba mengi ya kahawa Wilayani Mbozi katika Kata za Magamba, Nambinzo, Iyula na Igamba yameendelea kukauka. Ni lini Serikali itachimba mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji wa kahawa katika maeneo haya ambapo kahawa sasa inaendelea kukauka na hali imekuwa ni mbaya sana?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza sisi nchi yetu tunataka kwenda kwenye kilimo lakini kimekuwa na changamoto nyingi sana. Wizara yetu ya Maji na Umwagiliaji tumeona haja sasa ya kuingia katika kilimo cha umwagiliaji. Kama nilivyoeleza, tuna Tume yetu ambayo inapitia maeneo mbalimbali kubainisha yale maeneo ambayo tunaweza tukahakikisha kwamba tunajenga hayo mabwawa. Namwomba kaka yangu Mheshimiwa Haonga, sisi kama Wizara ya Maji na Umwagiliaji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi hao katika kuhakikisha tunatengeneza mabwawa hayo ili yaweze kuwa na faida kwa wananchi wao.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Waziri, Serikali imedhamiria kufanya kazi nzuri sana hasa katika Jimbo langu, imejenga bwawa na inajenga scheme ya umwagiliaji katika Bwawa la Ikagata, lakini kuna fedha kiasi cha shilingi milioni 180 na zaidi za scheme ya umwagiliaji ziliazimwa kwa ajili ya kuziba bwawa hili ambalo lilikuwa linavuja.
Je, ni lini Serikali itarudisha fedha katika mradi ule ili Mkandarasi aweze kulipwa, amalizie kazi hii ambayo dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano na Wizara yenu iko na nia njema kwa wananchi wa Jimbo langu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kwa ufupi tu nimwombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge saa saba mchana tuweze kukutana ili niweze kupata maelezo vizuri zaidi ili nami niweze kuhakikisha kwamba nalisimamia hili jambo liweze kukamilika kwa wakati. Ahsante.
MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nashukuru kwa mradi wa vijiji kumi katika kila Halmashauri, mradi wetu wa maji ule unakwenda vizuri.
Je, Serikali ina mpango gani katika vile vijiji ambavyo havitapitiwa na ule mradi wa vijiji kumi wa kuwachimbia visima virefu ili wananchi waweze kupata huduma ya maji safi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii nimjibu Mheshimiwa Mbunge wa Mkoa wangu wa Tanga, kaka yangu Mheshimiwa Mussa kwamba Wizara yetu ya maji kama nilivyoeleza, jukumu letu ni katika kuhakikisha tunawapatia wananchi maji mijini na vijijini na lengo la Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi ni kufikia asilimia 85 katika kuhakikisha vijijini wanapata maji. Sisi kama Wizara ya Maji tuna taasisi mbalimbali kwa maana ya DDCA katika kuhakikisha kwamba tunachimba visima hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mhandisi wa Maji katika Jimbo lake alete andiko, nasi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha tunawasaida wananchi wa Tanga. Ahsante.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Unavyoona Wabunge wamesimama ujue ndiyo hali ya maji nchini tatizo jinsi lilivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri wakati anajibu amekiri kabisa kwamba tatizo la maji lipo Wilaya ya Momba na sio tu Momba peke yake lipo nchi nzima. Sasa kauli mbiu ya ahadi ya kumtua mama ndoo kichwani imekuwa ngumu kweli kweli kutekelezeka kama ilivyo ahadi ya kupeleka milioni 50 kwa kila kijiji. (Makofi)
Je, Serikali inaweza ikatueleza kwa nini imekuwa rahisi kununua ndege ama Bombadier kuliko kupeleka maji safi na salama kwa wananchi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya mijini maji tunayotumia ku-flash kwenye vyoo ni bora kuliko maji ambayo wanatumia wananchi wa vijijini kwa sababu maji yale wananywea ng’ombe na wananchi wa kawaida wanakunywa huko huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini sasa Serikali isiwe na huruma kwa wananchi wa vijijini nchi nzima ili muweze kutatua hili tatizo la maji na sisi tuondokane na hii kero ambayo wananchi wamekuwa wanauliza kila siku wanahitaji maji safi na salama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza napenda nimjibu Mheshimiwa Mbunge kuwa Mungu anaposema kwamba yapaswa kushukuru kwa kila jambo, Serikali inafanya jitihada kubwa sana katika kuhakikisha inatatua matatizo ya maji. Tunaona miradi mikubwa ambayo inatekelezwa, tunatoa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka Tabora pamoja na miji ya Igunga, tunaona Mheshimiwa Rais anavyozindua miradi kila kukicha Nansio na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha tunwapatia wananchi maji kwa maana ya maji safi, salama na yenye kuwatosheleza na nimefanya ziara katika Mkoa wa Songwe kwa kuona changamoto hiyo, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni tisa na katika Jimbo lako tumetenga bilioni 1.77 katika kuhakikisha tunatatua tatizo hilo la maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kazi ya Mbunge ni kusimamia. Naomba asimamie fedha hizo katika kuhakikisha wananchi wako wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, lengo la Wizara yetu sio kuwapa wananchi maji masafi. Niwaombe sana wataalam wetu kwa maana ya wahandisi wa maji, wabuni miradi ambayo itakuwa na tija kwa wananchi wetu katika kuhakikisha wanapata maji yaliyo safi na bora ili kuhakikisha wanapata huduma hii muhimu.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Kwa kuwa upatikanaji wa maji safi na salama huathiri afya, muda wa uzalishaji na hivyo huathiri uchumi wa kaya au jamii kwa ujumla. Sasa Serikali yetu tunajua dhahiri kuna changamoto ya maji nchini.
Je, mnajua kwamba bila kutatua changamoto ya maji nchini hatutakaa kufikia lengo la uchumi wa kati 2020/ 2025? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwa maana ya kwamba tunatambua sasa hivi nchi yetu inaenda katika nchi ya viwanda kwa maana ya uchumi wa kati na tunajua kabisa maji ni rasilimali muhimu sana na maji hayana mbadala sio kama chai ukikosa chai labda utakunywa uji. Tunajua viwanda vinahitaji maji, wananchi wanahitaji maji, kwa hiyo tutaongeza jitihada kubwa sana katika kukarabati, kujenga na kuunda miradi mikubwa katika kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji na tuwe na vyanzo vya kutosha ili mwisho wa siku azma iweze kutimilika. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali la nyongeza kama ifuatavyo; vijiji vingi vya Wilaya ya Hanang havina maji na vile ambavyo vimebahatika kuchimbiwa visima, visima havijakamilika.
Je, Mheshimiwa Waziri ananiambia nini ili kuhakikisha vile visima vilivyochimbwa vinakamilika na wale waliobahatika kuwa na visima hivyo waweze basi kunywa maji na kutumia kwa matumizi mengine? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza napenda nimpongeze sana mama yangu Mheshimiwa Nagu amekuwa ni mtetezi mkubwa sana wa wananchi wake katika suala zima la maji. Amekuwa analipigania na amekuwa akifuatilia katika Wizara yetu ya Maji na Waziri wangu ambaye ni Mheshimiwa Kamwelwe aliwaagiza watu wa DDCA kwenda kuchimba visima vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie kwamba tutawaagiza watu wetu wa DDCA katika kuhakikisha vile visima wanavikamilisha kwa wakati, ili wananchi wako waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza. (Makofi)
MHE. ALLY S. UNGANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwanza tunashukuru Kibiti tumechimbiwa visima 12 vikiwa katika Kijiji cha Mtunda, Nyamisati, Mahege, Mlanzi na Kivinja A. Je, ni lini sasa Serikali itakamilisha miundombinu hiyo ili wananchi hawa wapate maji safi na salama?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwamba je, sasa Naibu Waziri yupo tayari kuongozana na mimi kwenda katika Wilaya Mpya ya Kibiti, ili kujionea adha ya wananchi wanayopata na ukizingatia sasa hivi Kibiti ni salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge binafsi, Mbunge anafanya kazi nzuri sana. Nataka nimhakikishie wananchi wa Kibiti kwamba Mbunge wao anatosha mpaka chenji inabaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge sisi Wizara yetu ya Maji tumeona haja ya kuusaidia Mji wa Kibiti na tumechimba visima 12. Kubwa sisi tunataka tukamilishe miundombinu ile, ili wananchi wale waweze kupata maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi jukumu letu katika kuhakikisha miradi ile tunaikamilisha kwa wakati, ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala la mimi kwenda Kibiti. Nataka nimhakikishie kwa kuwa, sasahivi Kibiti ni salama, mimi kama Naibu Waziri niko tayari kwenda kuambatana naye kuzungumza na wananchi.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Mheshimiwa Waziri katika majibu yake wataalam wanajibu kana kwamba bado Halmashauri ni moja lakini tuna Halmashauri mbili; Halmashauri ya Wilaya ina majimbo mawili ya Mwibara kwa Mheshimiwa Kangi na Bunda kwa Mheshimiwa Boniphace; Halmashauri ya Mji ina Jimbo moja tu la Ester Bulaya, Bunda Mjini. Sasa haya majibu waliyompa ni ya enzi zile za babu, za Wasira, sio kipindi hiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nauliza maswali yangu mawili ya nyongeza. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara kwenye Jimbo langu la Bunda alitembelea Kikundi cha Igebesabo kilichopo Kata ya Nyatwali ambacho kina mradi mkubwa wa umwagiliaji uliogharimu zaidi ya shilingi milioni 700. Pale wana changamoto ya mashine kubwa ya kusukuma maji ambayo yanatoka Ziwa Viktoria aliwaahidi atawasaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini ahadi hii itatekelezwa kwa sababu pia katika hicho kikundi kuna vijana kama wewe Mheshimiwa Waziri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Idara ya Umwagiliaji ina changamoto nyingi ikiwepo ya bajeti na vitu vingine, lakini kwa sasa hivi hawana gari la kuweza kufanya patrol katika miradi mbalimbali ya umwagiliaji katika Wilaya nzima ya Bunda. Ni lini sasa watawapatiwa gari ili sasa kilimo cha umwagiliaji Bunda kiweze kushamiri na vijana wengi graduates sasa hivi wamejiajiri wenyewe kwenye shughuli za umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze kwa maswali mazuri lakini kubwa ambalo nataka nimhakikishie, ahadi ni deni. Kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha tunaitimiza kwa wakati ili wananchi wake, kwa maana ya kile kikundi, waweze kupata mashine hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala zima la gari, ili mradi uwe bora na wenye tija kwa wananchi lazima kuwe na usimamizi na ufuatiliaji wa karibu. Kwa hiyo suala la gari ni jambo la muhimu sana. Niagize wataalam wetu wa Bunda kufuatilia kitendea kazi hiki na sisi kama Wizara ya Maji tutatoa ushirikiano wa dhati kabisa katika kuhakikisha kinapatikana.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Skimu ya Mwakijembe ambayo imetumia fedha nyingi kujengwa, zaidi ya shilingi bilioni moja, mpaka leo hii haijakamilika kwa kukosa mifereji ya umwagiliaji lakini vilevile kukosa bwawa na sasa tunashuhudia maeneo ya wananchi yakichukuliwa na Jeshi bila fidia yoyote. Je, Waziri yuko tayari kuja kufanya ziara mahsusi Jimboni Mkinga ajionee hali hii ili kuweza kutatua tatizo linaloikabili skimu ile?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie kaka yangu, Mheshimiwa Dunstan Kitandula, mimi kama Naibu Waziri wa Maji nipo tayari.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wakulima wa mbogamboga wa Wilaya ya Lushoto wanachimba vidimbwi vidogovidogo kwa ajili tu ya kunyeshea mazao yao. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha kwa kuwajengea mifereji hasa wakulima wa mabondeni hasa Mabonde ya Boheloi, Mshizii, Kwai, Milungui, Ubiri, Kwekanga, Mazumbai, Mlola, Mboi hadi Makanya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu, Mheshimiwa Shekilindi (Bosnia), kwa kazi nzuri anazozifanya katika Jimbo lake la Lushoto. Kubwa ambacho nataka nimwambie ni kwamba nchi yetu sasa hivi tunakwenda katika uchumi wa kati, tumeona haja sasa ya kulima kilimo cha umwagiliaji. Nimhakikishie kwamba sisi Wizara yetu ya Maji tumetenga shilingi bilioni 29.767 katika kuhakikisha tunawekeza katika kilimo cha umwagiliaji. Niwaombe tu wataalam wetu wa Lushoto wasilale, wamsaidie Mheshimiwa Mbunge katika kuhakikisha jambo lake linatimilika kwa wakati.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya Mawaziri wa Wizara hii kutembelea chanzo cha maji cha Mto Qangded kule Karatu ambacho kinatumiwa na wananchi katika kilimo cha umwagiliaji zaidi ya vijiji sita. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri, yuko tayari sasa kutimiza ahadi yake ya kutembelea eneo hilo ili kutatua changamoto ambazo wakulima wa eneo hilo wanakumbana nazo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nilihakikishie Bunge lako niliahidi kwenda kutembelea Jimbo la Karatu lakini kutokana na changamoto sikuweza kufanikisha ahadi ile. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kabla ya Bunge la Novemba tutatimiza ahadi ile kwa kuhakikisha tunatembelea miradi katika jimbo lake.
MHE. LUCY S.MAGERELI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru na nimeshukuru kupata majibu ya Serikali, lakini...
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijauliza maswali yangu mawili ya nyongeza naomba nitoe maelezo mafupi ya utangulizi kwamba ni fedheha na ni mambo ya aibu kabisa kwa Jiji kongwe kama Dar es Salam kwa Mji Mkuu wa biashara wa muda mrefu tangu uhuru wa nchi hii kupatikana kuendelea kuteseka na adha ya maji mpaka leo hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu ya Serikali anazungumzia habari ya visima 20 ambavyo vinachimbwa Mpera na Kimbiji. Kwa bahati mbaya ni kwamba visima hivyo mpaka sasa havijakamilika kwenye zoezi la kuchimbwa.
Je, fedha wanazosema wanatafuta, zinatafutwa kutoka wapi na zitapatikana lini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwenye majibu ya Waziri anasema katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imepanga kukamilisha miradi ya viporo kama kipaumbele. Tunavyozungumza bajeti 2017/2018 inakwisha siku chache sana zijazo na bado….
Mheshimiwa Mwenyekiti, swala hili linaitwa kipaumbele. Je, Mheshimiwa Waziri anajibu tofauti kwenye swali (b)?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwenyezi Mungu anasema unapaswa kushukuru kwa kila jambo na usipowashukuru binadamu hata Mwenyezi Mungu unaweza hutamshukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kabisa Jiji la Dar es Salam lilikuwa na changamoto kubwa sana ya maji, lakini mpaka sasa asilimia 78 ya wananchi wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. Watu wa Mamlaka ya DAWASCO wana mpango mkubwa mkubwa wa kuongeza mtambo ile wa Ruvu juu na Ruvu chini katika kuhakikisha wananchi wa Dar es Salaam wanaendelea kupata maji, safi salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa katika maeneo ya viunga vya Dar es Salam kwenye changamoto ya maji Serikali imeshachimba visima 20 na sasa tumejipanga katika kuhakikisha tunasambaza maji ili wananchi wa Ukonga na maeneo mengine waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miradi ya viporo, kazi inaendelea kufanyika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kutuamini na sisi katika yale maeneo ambapo tunahitajika kukamilisha viporo vile tutaendelea kuvikamilisha kwa wakati, ahsante sana.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
Nina swali moja tu la nyongeza; kwa kuwa maji ni siasa, maji ni uchumi, na maji ni maendeleo; na kwa kuwa Serikali ilikuwa na mipango ya kuchimba visima vya maji katika Kijiji cha Majami, Nana, Mafuto, Lupeta 30, Makutupa pamoja na Ngalamilo na walielezwa kabisa fedha zilizotengwa kwa ajili ya visima hivyo.
Je, ni lini sasa Serikali watakwenda kuanza kuchimba visima vya maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Wizara yetu ya Maji ni katika kuhakikisha wananchi wanapata maji safi, salama. Nimuombe sana Mheshimiwa Mbunge mimi kama Naibu Waziri wa Maji nipo tayari kufanya cross check na watu wa DDCA waende mara moja katika kuhakikisha wananchi wake wa Mpwapwa wanapata safi, salama na yenye kuwatosheleza, ahsante sana.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali ina mpango wa kurekebisha na kuvitibu visima viporo ambavyo mpaka leo havijatengenezwa.
Je, Serikali inasema nini sasa kuhusu visima vyangu virefu ambavyo vimetengenezwa miaka sita iliyopita mpaka leo havijarekebishwa, ambavyo ni, Kisima cha Tupindo, kilichopo Kata ya Mbede na Kisima cha Kibaoni ambavyo mashine zake zimedumbukia ndani na vimetumia kutengezwa takribani pesa za Serikali milioni 800?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kazi kubwa inayofanywa na mama yangu Kikwembe. Nimuombe tu kwa kuwa Wahandisi wote wapo bado Dodoma, labla baada ya saa saba afike na Mwandisi wake ili tuangalie namna gani tunaweza tukamsadi katika kutatua tatizo la maji.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri; kwa sababu Jimbo la Sumve lina visima 89 ambavyo ni vibovu havitoi maji, na barua unayo; je, ni lini visima hivyo sasa vitatengenezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti,...
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua changamoto hizo na viporo mbalimbali Waziri wangu akaona haja sasa kwa Wabunge wote kupitisha barua kuangalia namna gani na kuorodhesha maeneo ambayo yenye changamoto. Labla nimuombe Mheshimiwa Mbunge jambo hili baada ya kulichukua tutalifanyia kazi kwa wakati na yeye katika maeneo yake hatomuacha katika kuhakikisha tunamrekebishia visima vyake, ahsante sana.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Ndanda limegawanyika katika maeneo matatu ya mtandao wa maji. Kuna upande wa Mashariki ambao unaanzia Kata ya Nanganga mpaka Chikukwe kwenyewe kuna mradi mkubwa wa maji unafanyika pale. Kata ya Magharibi kwenye Vijiji vya Chingulungulu…
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, sasa hivi Serikali imeanzisha utaratibu wa kuchimba mabwawa kwa ajili ya maji na kuendeleza mabwawa ya zamani ikiwepo bwawa lililoko Kata ya Lukuledi. Nataka kufahamu kutoka kwa Waziri kwa sababu maji safi na salama yanayotokea bomba la Mbwinji yamefika mpaka Kata ya Chikunje ambapo ni kilomita 10 tu kufika kwenye Kata ya Lukuledi. Je, Serikali haioni haja ya kuendeleza mradi huu wa maji badala ya kwenda kuendeleza lile bwawa ambalo halina chanzo cha uhakika cha maji zaidi ya maji ya mvua?
NAIBU WAZIRI WA WIZARA YA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu lengo lake ni kuhakikisha wananchi wanapata maji. Kwa ushauri wa Mheshimiwa Mbunge kama kuna chanzo cha uhakika, tunaweza kuweka utaratibu kuhakikisha wananchi wako wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pia nashukuru kwa majibu ya Serikali. Nitakuwa na swali moja tu la nyongeza. Kata ya Litumbandyosi iliyopo Wilayani Mbinga inakabiliwa na uhaba mkubwa wa upatikanaji wa maji safi na maji salama. Je, ni lini Serikali itakamilisha miradi ya visima virefu katika Kijiji cha Kingoli, Luhagara, Mabuni na Litumbandyosi? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri. Vile vile nilishukuru sana Bunge lako Tukufu limetuidhinishia bajeti na katika bajeti tuliyoidhinishiwa Mbinga tumeitengea Sh.1,773,000,000 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nimwombe Mhandisi wa Maji wa Mbinga asilale atumie zile fedha katika kuhakikisha anatatua tatizo la maji kikiwemo Kijiji cha Kingole. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. RHODA E. KUMCHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Nataka niulize swali moja la nyongeza kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Manispaa ya Mpanda imekuwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama na kutokana na ongezeko kwamba kwa sasa hivi ni Manispaa kumekuwa na changamoto hiyo na Idara ya Maji wamekuwa hawatoi taarifa kwamba ni lini watakata maji au ni lini maji yanaweza kuwa yanapatikana kwa wingi. Sasa nini tamko la Serikali kuhakikisha kwamba wakazi wa Manispaa ya Mpanda wanapata maji kwa wingi na yanawatosheleza wakazi hao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na pia nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali nzuri. Kikubwa sisi kama Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha wananchi wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. Nimepokea changamoto hiyo na namhakikishia Mheshimiwa Mbunge nitalifuatilia ili tuweze kuhakikisha watanzania wale wa Mpanda wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kutokana na swali la msingi lililoulizwa kuhusu Dar es Salaam naomba Wizara ya Maji ituambie kwa sababu baada ya Ruvu Chini na Ruvu Juu kukamilika sasa katika Jiji la Dar es Salaam maji yanamwagika sana karibu asilimia 40. Serikali ina mkakati gani wa kuweza kuondoa umwagikaji wa maji ili kuisaidia pesa ile ikarudi Serikali.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kuhusu suala zima la upotevu wa maji. Serikali imekuwa ikiwekeza fedha nyingi sana katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji. Hata hivyo, ipo hali ya kuona upotevu mkubwa wa maji barabarani ama mitaani na kuwa si hali nzuri sana kuona wananchi hawana maji lakini maji yanapotea.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wangu aliagiza Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Maji na kufanya nao kikao na akawagiza kujenga na kutengeneza miundombinu ambayo rafiki ambayo itakayoweza kudhibiti upotevu wa maji mpaka kufikia kiwango kile cha kimataifa cha asilimia 20 ambacho kinakubalika. Kwa hiyo, Serikali inaendelea na jitihada katika kujenga na kukarabati katika suala zima la kudhibiti upotevu wa maji.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Pamoja na shukrani za wananchi wa Bagamoyo kwa Mheshimiwa Waziri kwa kutujengea tanki kubwa la lita milioni sita Bagamoyo Mjini. Naomba kuuliza swali moja kwamba ni lini sasa Wizara itaanza mradi wa kusambaza mtandao wa mabomba ya maji ili maji hayo sasa yaweze kuwafikia wananchi katika Mji wa Bagamoyo na Kata zote katika Jimbo la Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri na nia njema ya kuhakikisha wananchi wake wa Bagamoyo wanapata maji safi, salama ya yenye kuwatosheleza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa kuwa suala hili la maji ni la uhitaji mkubwa sana tutalifanya kwa haraka ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naipongeza na kuishukuru sana Serikali kwa kutoa fedha za kuweza kuimarisha upatikanaji wa maji Mji wa Kateshi ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Hanang na wenyewe viongozi wapo hapo Gallery, naomba Mheshimiwa Waziri atuhakikishie kwamba ifikapo mwezi wa tisa ambapo ni ukame na hamna maji Kateshi kama maji hayo yatapatikana na nitaishukuru zaidi Serikali. Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya na amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana katika suala zima la maji katika Mji wa Kateshi. Kubwa nimhakikishie utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, Serikali imeshatafuta fedha na imeshapata. Kwa hiyo, nimwombe Mhandisi wa Maji afanye kila linalowezekana katika kuhakikisha wananchi hawa ndani ya mwezi wa Tisa wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
Mheshimiwa Spika, lingine nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya Bunge nitafika Kateshi katika kuhakikisha tunaongeza msukumo ili wananchi wake waweze kupata maji safi. (Makofi)
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru na nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Serikali ilikuwa bado haijaupa kipaumbele mradi huu na sasa wanasema walishaliweka katika vipaumbele vya kutekeleza mradi huu kama mradi kabambe wa umwagiliaji. Je, sasa Waziri atakuwa tayari kufuatana na Mbunge wa Jimbo ndugu yangu Stephen Ngonyani baada ya Bunge hili ili kwenda kuwaeleza wananchi wa Mkomazi kutokana na mradi huu kuwa unasuasua kwa muda mrefu?
La pili, kwa kuwa atakapokuwa anapita kwenda Mkomazi, kwa kuwa kauli mbiu ya Rais wetu mpendwa ni Hapa Kazi tu, je, atakuwa tayari kupita Korogwe Mjini kwenye mradi wa kwa Mgumi wa umwagiliaji ili aweze kwenda kuuona na hatimaye kuweza kuufanyia kazi kutokana na matatizo walionayo? (Makofi). Mheshimimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, natambua kazi nzuri sana inayofanywa na Mheshimiwa Mbunge Hillary Ngonyani, Maji Marefu, kaka yangu, nataka nimhakikishie kwamba striker haogopi back. Kama Mbunge wa Jimbo la Pangani na Naibu Waziri wa Maji nipo tayari kwenda kuzungumza na wananchi wa Korogwe katika kuwahakikishia kwamba kilimo cha umwagiliaji kitafanyika katika eneo lake.
Mheshimiwa Spika, lingine nimhakikishie Mheshimiwa mama yangu Mary Chatanda tumekwisha kubaliana baada ya Bunge hili nitapita Kateshi, nitapitia Mkoa wa Tanga kufanya ziara yangu kuhakikisha wananchi wa Mkoa wangu wa Tanga wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa katika Wilaya ya Mpwapwa na Kongwa kuna skimu za umwagiliaji ambazo zilijengwa sasa ni miaka 10 hazijafanyiwa ukarabati, katika Kijiji cha Chamkoroma, Mseta, Tumbugwe, Mlembule, Boli na Injovu. Hakuna hata mtaalam mmoja ambaye amepitia kuziona skimu zile. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kwenda kukagua skimu za umwagiliaji katika maeneo haya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa kutambua sasa hivi tunaelekea katika uchumi wa viwanda na uchumi wa viwanda unategemeana kabisa na kilimo cha umwagiliaji. Nipo tayari Mheshimiwa Mbunge kuongozana na yeye katika kuhakikisha tunakwenda kuziangalia skimu zile zake za umwagiliaji.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi hii. Kwa kuwa Kata ya Mkomazi ni jirani sana na Kata Ndungu na kwa kuwa pale kwenye Kata Ndungu kuna skimu kubwa sana ya umwagiliaji ambayo inasaidia kilimo kikubwa cha mpunga. Skimu ile sasa imeonekana kwamba imechoka sana na maisha ya wananchi wa Kata ya Ndungu, Kihurio mpaka Kalemawe yapo hatarini; je, Mheshimiwa Waziri atakapotoka Korogwe pale Mkomazi kwa sababu Ndungu ni jirani anatuambia nini, atakuja kuona skimu ile?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nirudie tena ukisoma Tenzi za Rohoni inasema unapotembea na kuzuru wengine naomba usinipite Mwokozi, sitompita Mheshimiwa mama Anne Kilango katika kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. (Makofi/Kicheko)
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza. Utaratibu wa Serikali wa kutekeleza miradi ya maji ni ule ambao unamtaka Mkandarasi atekeleze alete madai na aweze kulipwa. Lakini utaratibu huu umeonesha kwamba Wakandarasi wengi hawana uwezo matokeo yake miradi mingi inachelewa sana kutekelezwa na mingine inaharibika. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha utaratibu wa utekelezaji wa miradi wa maji inayoanza kuanzia tarehe 1 mwezi wa 7 ukiwemo huu mradi wa maji wa Makambako?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, mkopo nafuu kutoka Serikali ya India unahusu pia vilevile Mji wa Njombe ambao upembuzi yakinifu umefanyika kwa ajili ya kupata maji kutoka chanzo cha Mto Hagafilo na kusambaza katika Mji wa Njombe na sasa huu ni mwaka wa tatu, kila mwaka Serikali inatuambia kwamba mradi huu unaanza. Je, Serikali inatoa majibu gani ya uhakika sasa kuwahakikishia wananchi wa Mji wa Njombe kwamba mradi huu wa maji kutoka Mji wa Hagafilo unaanza kutelekezwa? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, pamoja na nia njema ya Wizara yetu ya Maji katika kuhakikisha Watanzania wanapata maji safi, salama na yenye kutosheleza, lakini imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo la Wakandarasi.
Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuona haja sasa Wahandisi wote wa maji kutoka Halmashauri waje kuweka katika Wizara yetu ya Maji ili tuwe na usimamizi wa ukaribu na majukumu ya pamoja katika kuhakikisha tunatatua matatizo hayo. Kwa hiyo, mkakati wa Serikali ni kuanzisha sasa Wakala wa Maji Vijijini katika kuhakikisha Watanzania waliokupo vijijini wanafikiwa na asilimia 85 ya upatikanaji wa maji.
Mheshimiwa Spika, pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, kama nilivyomhakikishia kwamba tumeshasaini mkataba ule wa kupata fedha, niwahakikishie wananchi wa Njombe kwamba watapata maji hayo safi, salama na yenye kuwatosheleza. Sisi kama viongozi wa Wizara tutasimamia kwa ukaribu ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika Jimbo langu la Ulanga Kijiji cha Gombe kuna mradi mmoja mradi wa kiinimacho. Mawaziri wote anapokuja Waziri maji yanajazwa kwenye tanki usiku kucha, akija Waziri asubuhi anakuta yanatoka. Kaja Waziri kafanyiwa hivyo hivyo, kaja Naibu Waziri kafanyiwa hivyo hivyo. Sasa Mheshimiwa Waziri anatoa kauli gani kuhusiana na mradi huu kiini macho ambao unafanya wananchi wanashindwa kupata maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nilifanya ziara katika Jimbo la Ulanga na tumefika katika eneo lile tumeona hali ya utekelezaji na moja ya majukumu nilichukua hatua ya kuhakikisha yule Mkandarasi anakamatwa kwa sababu ya kusuasua kwa utekelezaji wa mradi ule. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge nipo tayari kukutana naye leo baada ya saa saba tuangalie wapi walikofikia ili mwisho wa siku na sisi tuendelee kuongeza nguvu wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Spika, kwa kweli nashukuru sana kwa kuniona maana yake nikasema mbona ni mrefu kuliko wote lakini nimesimama mara 20. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Spika, nataka kumuuliza swali moja la nyongeza Mheshimiwa Naibu Waziri. Nakumbuka mwezi Machi alikuja Songwe Wilaya mpya tulikuwa naye kwenye Kata ya Chang’ombe, Kijiji cha Chang’ombe na Mbuyuni na yeye mwenyewe aliona ufisadi wa maji katika mradi wa Chang’ombe uliokuwa unashikiliwa na Mkurugenzi Chunya na sasa ni Wilaya Mpya na aliniahidi kwamba atafuatilia kumrudisha yule Mkandarasi aje amalizie ule mradi wa maji Chang’ombe, lakini mpaka leo kimya. Nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli nilishafika katika Halmashauri ya Songwe na tumeona changamoto hiyo na nilikwishatoa maagizo kwa Mhandisi wa Maji katika suala zima la kusimamia. Nimwombe Mhandisi wa Maji wa Songwe asimamie maagizo ambayo niliyompa na kama ameshindwa basi ajitathmini, kwa sababu sisi tunachotaka ni kazi na wananchi wale waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba kuna tatizo la maji kwa wananchi wa maeneo ya Rombo na suala hili limekuwepo tokea miaka ya 1960, ni lini Serikali itaruhusu uchepushaji wa hayo maji ili wananchi wa Rombo ambao wanapata maji kutoka Mlima Kilimanjaro kwa wingi sana waweze kutatua tatizo hilo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa suala la Rombo linafanana kabisa na suala la Ubungo, hasa katika maeneo ya Kajima, Kimara na Makoka, je, ni lini Serikali itawasaidia wananchi wa Ubungo kukamilisha mradi mkubwa wa maji ambao umetokea Kibamba hadi maeneo hayo ya Kimara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, lakini natumia nafasi hii kutambua kwamba tuna changamoto kubwa sana katika maeneo mbalimbali kuhusu suala zima la maji. Serikali kwa kuona haja ya kutatua changamoto hii ya maji, katika Wilaya ya Rombo tumetenga kiasi cha Sh.1,530,000,000 ili kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Ubungo nilifanya ziara pamoja na Mheshimiwa Mbunge na kuna mradi mkubwa wa upanuzi ili kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. Kubwa, mimi kama Naibu Waziri pamoja na viongozi wote wa Wizara tutausimamia mradi huu ili kuhakikisha wananchi wake wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kata ya Kapalamsenga iko jirani na Ziwa Tanganyika lakini haina maji kabisa. Ni lini Serikali itatatua tatizo la kata hiyo kwa kupeleka maji kwa kuyatoa Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tunatambua kabisa unapokuwa karibu na waridi lazima unukie. Labda nimwombe Mheshimiwa Mbunge tukutane tushauriane na Mkurugenzi wa eneo husika, tuangalie ni kwa namna gani tunaweza tukabuni mradi katika kuhakikisha wananchi wake wa kata hiyo wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kabla ya kuuliza swali naomba uniruhusu niwape pole wananchi wa Jimbo la Buyungu kwa kupoteza Mbunge wao. Naomba wawe watulivu katika kipindi hiki kigumu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mji wa Kakonko bado lipo tatizo kubwa la upatikanaji wa maji. Katika mji huo maji hutoka mara tatu kwa wiki katika visima viwili; kimoja ni kisima cha Mbizi ambacho kinatumia pampu na cha pili ni kisima cha Kanyovi kinachotumia solar. Nashukuru Serikali katika bajeti hii kwa kutupangia pesa. Je, ni lini sasa mradi huo utaanza katika Mji wa Kakonko? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna ya kipekee anavyowapigania wananchi wake katika suala zima la maji. Nitumie nafasi hii kulishukuru sana Bunge lako Tukufu kwa kutuidhinishia kiasi cha Sh.727,345,000,000 yote hii katika kuhakikisha tunaenda kutatua tatizo la maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya bajeti hii kuu kupitishwa sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. (Makofi)
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa majibu mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kero ya maji katika Mkoa wa Singida ni ya muda mrefu na hii ni kutokana na jiografia yake ya hali ya ukame. Je, Serikali ina mpango gani wa kuchimba mabwawa katika Mkoa wa Singida ili kupunguza makali ya kero hii? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa upatikanaji wa maji katika vijiji 13 vya Jimbo la Manyoni Mashariki vikiwemo Mangoli, Ikasi, Magasi, Winamila na Ipanduka imekuwa ni kero kubwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuchimba visima katika vijiji hivyo ili kuwawezesha wananchi kupata maji safi na salama na kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana dada yangu Mheshimiwa Aisharose, amekuwa ni mpiganaji na amekuwa ni mfuatiliaji wa mara kwa mara katika Wizara yetu ya Maji katika kuhakikisha wananchi wake wa Mkoa wa Singida wanapata maji safi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua eneo la Singida ni kame, Wizara yetu imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali katika kuchimba visima virefu na hata mabwawa katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, wanasema unapotembea na kuzuru wengine naomba usinipite, hatutampita katika kuhakikisha wananchi wa Singida wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, Serikali imekuwa ikitekeleza miradi ya maji kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji lakini mpaka sasa miradi 1,469 imekamilika kati ya miradi 1,810. Mkakati wetu wa Wizara ni katika kuhakikisha tunatekeleza miradi 387. Nimhakikishie dada yangu katika miradi hiyo sisi kama Wizara ya Maji tutampa ushirikiano mkubwa sana katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji katika vijiji alivyoviorodhesha.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Serikali katika kutekeleza miradi mbalimbali maji ya Benki ya Dunia, viko vijiji ambavyo vilikuwepo kwenye mpango kikiwemo kijiji cha Nakapanya, Majimaji, Muwesi na Mchoteka. Vijiji hivi viliwekwa kwenye mpango na ilionyesha kwamba pesa yake ipo lakini majibu ya Serikali walisema kwamba vyanzo havijapatikana. Nini sasa kauli ya Serikali katika kuendelea kufanya utafiti ili wananchi wale wafaidike na huo mradi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana lakini nampongeze Mheshimiwa Mbunge, siyo mara yake ya kwanza kuulizia kuhusu suala zima la maji. Kama fedha zipo, namwomba sana Mhandisi wa Maji wa eneo hilo afanye kazi. Unapokuwa Mhandisi wa Maji, jukumu lako ni katika kuhakikisha wananchi wanapata maji. Sisi kama Wizara ya Maji tuko tayari hata kutoa watalaam wetu katika kuhakikisha wanatafuta vyanzo vya maji ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Mradi wa maji wa Bukindo, Kagunguli Visiwani Ukerewe unatekelezwa kwa ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais na kusimamia na MWAUWASA. Mradi ule kwa sehemu kubwa umekamilika lakini haujaanza kutoa huduma kwa sababu ya kukosa pesa za kuunganisha umeme. Je, Serikali iko tayari kuwasiliana na MWAUWASA ili waweze kusaidia uunganishaji umeme mradi huo uweze kutoa huduma uweze kuwasaidia wananchi wa Kata za Bukindo, Kagunguli na Mtungulu ambao watafaidika na mradi huu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji tupo tayari kufanya mawasiliano na Mkurugenzi wa MWAUWASA na ikatakapobidi tufanye jambo hili la haraka ili wananchi wake waweze kupata umeme ili mradi uweze kutekelezeka na wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Mji wa Bukoba una maji mengi kutokana na Serikali kufanya vizuri, lini Wilaya ya Misenyi itapata maji kutoka kwenye chanzo cha Bukoba Mjini kwa sababu hawana uwezo wa kutumia yale maji yote?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nampongeza mzee wangu Mheshimiwa Bulembo. Moja, nimhakikishie maeneo ambayo sijawahi kufika ni Bukoba, baada ya Bunge hili nitafika Bukoba tunaangalie hali halisi na namna gani tunaweza tukashauriana kuweza kutatua tatizo la maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji, kama nilivyoeleza, Bunge lako Tukufu limetuidhinishia bajeti yetu Sh.727,345,000,00, yote hii ni katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Sisi Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kikubwa Waheshimiwa Wabunge, tunaomba ushirikiano wa dhati katika kusimamia na kufuatilia miradi hii ya maji ambayo tunatekeleza katika maeneo yao.
MHE. ALLY M. KEISSY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Lini mradi wa maji ambao ulipatikana kwa njia ya ufisadi katika Kijiji cha Kamwanda, Kirando utaanza? Maana yake wananchi mpaka sasa wanasubiri, siyo kosa lao, wanateseka siyo kosa lao, wananyanyaswa siyo kosa lao. Lini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na nia njema ya Serikali katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji na imekuwa ikipeleka fedha nyingi maeneo mbalimbali, lakini kumekuwa na ubabaishaji na wakati mwingine hata baadhi ya wakandarasi kufisadi fedha za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilifanya ziara katika Jimbo la Mheshimiwa Keissy tukagundua ufujaji fedha zile, tukahakikisha kwamba TAKUKURU wanachukua hatua. Sasa hivi kuna hatua mbalimbali ambazo zinachukuliwa na vyombo hivi vya dola. Namwomba nimweleze Mheshimiwa Keissy, katika kipindi hiki sisi kama Wizara ya Maji tutahakikisha wananchi hawa wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza wakati Serikali ikiendelea na suala zima la kuwashikilia wale watu ambao wanawatuhumu.
MHE. BALOZI ADADI. M.RAJABU: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza: Kwanza napenda kuwapongeza sana Mawaziri wote yeye Naibu Waziri ameshafika Muheza pamoja na Waziri mwenyewe wiki iliyopita Ijumaa alikuwa Muheza na ameonesha ishara kwamba kweli Muheza inakaribia kupata maji. Isitoshe pia Mwewe katika kipindi cha Clouds TV imesema kwamba Muheza itapata maji hivi karibuni.
Mheshimiwa Spika, mradi huu wa Zigi kutoa maji kutoka Mto Zigi mpaka Mjini Muheza ni kati ya miradi 17 ambayo tunategemea kupata mkopo wa Serikali ya India ya dola milioni 500. Nataka kujua mradi huu utaanza lini?
Mheshimiwa Spika, la pili, pale Muheza Halmashauri ya Wilaya imenunua mtambo wa kuchimba visima, lakini mtambo huu tunashindwa kuutumia kikamilifu kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Kwenye bajeti hii ya wakati huu tumepangiwa zaidi ya bilioni moja na tuna mpango wa kuchimba zaidi ya visima 50, Halmashauri imekwishapitisha.
Mheshimiwa Spika, nataka Waziri awahakikishie wananchi wa Muheza kwamba Urasimu utaondolewa, tunataka kuchukua kiasi cha fedha kutoka kwenye hiyo bilioni ambayo tumepangiwa ili tuweze kutumia mtambo huu ili tuweze kuchimba visima. Nataka Mheshimiwa Waziri awahakikishie wananchi kwamba urasimu huo utaondolewa na utasaidia ku-facilitate mipango hii iweze kuendelea.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri, lakini niwahakikishie wananchi wa Muheza wana Mbunge mfuatiliaji.
Mheshimiwa Spika, kwa kudhamiria kwa kutatua tatizo la maji kabisa katika Mji wa Muheza tumeona haja ya kuwekeza mradi mkubwa wa maji kati ya miradi ile 17 na utekelezaji wa maji inategemea na upatikanaji wa fedha. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mpaka sasa Serikali imeshasaini mkataba na ile Serikali ya India mradi wa mkopo wa milioni 500 katika kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie yeye pamoja na wananchi wa Muheza wakati wowote mradi ule utaanza mara moja. Sisi kama Wizara ya Maji tutasimamia na kufuatilia fedha zile mradi uanze mara moja na kwa wakati katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo lakini tuwapongeze kwa kununua mtambo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge leo saa saba tukutane na Katibu Mkuu wa Maji ili katika kuhakikisha namna gani tunaweza tukawasaidia wananchi wa Muheza waondokane na tatizo hilo la maji katika kuhakikisha tunawaunga mkono. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; katika Kata ya Mwilamvya ndipo yalipo machinjio ya ng’ombe, mbuzi na kondoo. Eneo hilo hupata maji mara mbili kwa wiki au mara tatu, lakini hivi sasa ninavyoongea eneo hilo halina maji na ni muda wa mwezi mzima maji hayapatikani katika eneo hilo.
Je, Serikali iko tayari kutoa pesa kwa mpango wa dharura ili eneo hilo la machinjio liweze kupatiwa maji? (Makofi)
Swali langu la pili, katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu DC ipo miradi ya maji ambayo haijakamilika, imefikia asilimia 85 mpaka 95 lakini imekwama kwa ajili ya ukosefu wa pesa; je, ni lini sasa Serikali itamalizia miradi hiyo kwa kupeleka pesa ili miradi hiyo iweze kukamilika na wanawake waweze kuondolewa adha ya upatikanaji wa maji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Awali ya yote nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge, ni mama shupavu, jasiri, mfuatiliaji na mhangaikaji wa matatizo ya wananchi wa Kigoma hasa katika suala zima la maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wako wa Mwilamvya hususan katika eneo hilo la Machinjio katika kuhakikisha wanapata maji safi ili waendelee na usafi, wakati mwingine usafi ni uhai wa mwanadamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kuhusu suala zima la miradi ambayo haijakamilika, nitumie nafasi hii kulishukuru Bunge lako tukufu na wewe mwenyewe kwa Wizara yetu ya Maji kuidhinishiwa fedha na katika Mji huo wa Kasulu umetengewa kiasi cha shilingi 1,466,000,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na sisi Wizara na viongozi katika kuhakikisha tunasimamia fedha zile ili ziende zikamilishe miradi ambayo haijakamilika ili wananchi wake waweze kupata maji, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. AZZA H. HAMAD: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza. Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga hawana mradi hata mmoja wa umwagiliaji na hivyo kuwepo kwa mradi huu tulitegemea kuleta tija kwa wakulima wetu, hasa wakulima wa mbogamboga na vitunguu.
Mheshimiwa Spika, mradi huu umetumia fedha nyingi sana na umeachwa na mashimo mengi ambayo hayana maana yoyote kwa wakulima wetu. Swali la kwanza, je, Serikali ipo tayari sasa kutoa kipaumbele katika mradi huu ili uweze kuleta tija kwa wananchi kama ambavyo Serikali ilikuwa imekusudia.
Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Mheshimiwa Naibu Waziri, yuko tayari sasa kwenda katika Kijiji cha Ishololo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga akajionee mwenyewe hali halisi ambayo iliachwa na Mkandarasi pamoja na fedha nyingi kutumika katika mradi ule? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, ni Mbunge mfuatiliaji, ni mpambanaji wa matatizo ya wananchi wake wa Shinyanga, lakini kubwa la msingi kwa kuzingatia umuhimu wa umwagiliaji, Serikali itatoa kipaumbele katika suala zima umwagiliaji katika Kijiji cha Ishololo katika kuhakikisha wananchi wa Shinyanga wanawekeza katika umwagiliaji ili tupate bidhaa au fursa ambayo itaweza kuwekeza katika suala zima la viwanda.
Mheshimiwa Spika, la msingi lingine ambalo ameniomba nifike katika eneo la Ishololo, niko tayari, mimi ama Waziri wangu tumejipanga katika kuhakikisha Bunge litakapokuwa limekwisha, kutembelea maeneo yote ambayo tuliahidi Waheshimiwa Wabunge kufika ili kujionea changamoto na maeneo yote ambayo tutakuta yana changamoto tutachukua hatua.
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kutokana na swali la msingi lililoulizwa na Mheshimiwa Azza, kule Mkoani Mara kuna Wilaya moja inaitwa Serengeti, katika ile Wilaya ya Serengeti kuna Bwawa moja linaitwa Manchira, limeanza tangu mwaka 1988, mpaka leo maji hayatoki unaambiwa kuna chujio. Naomba tamko la Serikali, lini maji yale yataanza kutoka kuwasaidia wananchi wa Serengeti, maana ni miaka 10 leo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, hakuna jambo lisilokuwa na mwisho na sisi kama viongozi wa Wizara hii ya Maji, jukumu letu ni kuhakikisha Watanzania wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge Baba yangu Mzee Bulembo, hebu tuonane tuweze kupata mawazo ya pamoja ili tuweze kusukuma katika kuhakikisha wananchi wale wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi asubuhi hii. Naomba niungane na Mheshimiwa Azza, naomba niulize swali moja dogo la nyongeza. Wilaya ya Mvomero imejaaliwa baraka kubwa na Mwenyezi Mungu, maji ni mengi, mabonde ni mengi, Waziri alituahidi miradi miwili ya umwagiliaji. Mradi wa Mbogo na mradi wa Kigugu yenye thamani ya shilingi bilioni tatu toka mwaka jana. Je, ni lini sasa fedha hizo zitatolewa ili wananchi wale waweze kujiendeleza katika miradi hii ya umwagiliaji. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Ni kweli aliahidiwa na Mheshimiwa Waziri wangu kupewa miradi miwili ya umwagiliaji na kwa kuwa ahadi ni deni, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sasa hivi tunapitia mapitio ya mpango kabambe wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ili tuweze kujiridhisha. Nataka nimhakikishie ahadi ile tutaitekeleza katika kuhakikisha wananchi wake wa Mvomero wanapata miradi hiyo yote miwili ya umwagiliaji.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza. Bonde la Mto Ruhuhu ambalo linaunganisha Wilaya ya Ludewa na Wilaya ya Nyasa, liliwekwa kwenye bajeti ya 2016/2017 juu ya ujenzi wa bwawa la umwagiliaji. Cha kushangaza, katika miaka hii miwili bwawa lile halipo kwenye bajeti. Je, Serikali ina mpango gani na ujenzi wa Bwawa la Mto Ruhuhu.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, tunatambua umuhimu wa umwagiliaji, lakini katika suala zima la umwagiliaji tangu tumeingia katika Wizara hii tumekuta changamoto kubwa sana. Kutokana na changamoto tulizobainisha katika umwagiliaji, Waziri wangu akaona haja sasa ya kupitia mpango kabambe wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ya mwaka 2002 ili tuweze kubainisha zile changamoto na kuweza kuzipatia majibu.
Mheshimiwa Spika, tumeona baadhi ya miradi ya umwagiliaji imejengwa lakini haijakamilika, vile vile hata hiyo iliyokamilika imekuwa ikiwasaidia wakulima katika kuvuna msimu mmoja wakati tunapozungumzia umwagiliaji ni mbadala kwa maana ya wakulima waweze kulima kiangazi na hata masika.
Mheshimiwa Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, baada ya mapitio, sisi kama Wizara ya Maji na Umwagiliaji, tutaona umuhimu wa kuhakikisha kwamba tunampa kipaumbele, wananchi wake waweze kupata kilimo cha umwagiliaji.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Spika, naskushukuru sana. Naomba na mimi niulize swali la nyongeza. Skimu nyingi za umwagiliaji ambazo ziko Mbozi, Kata ya Bara kuna Skimu ya umwagiliaji ambayo ni ya miaka mingi sana, miundombinu yake imechoka na skimu hii haifanyi kazi vizuri. Sasa Mheshimiwa Waziri yuko tayari kukarabati skimu hii ya umwagiliaji ambayo iko Kata ya Bara ili iweze kuwasaidia wananchi wa Kijiji cha Bara, Kata ya Bara, Wilaya ya Mbozi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Spika, awali ya yote kama nilivyokuwa nimeeleza kwamba, katika Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji tumeona kabisa tumekuwa na changamoto katika suala zima la umwagiliaji. Moja ya changamoto tumekuwa na miradi mingi lakini haijakamilika, tunapitia mapitio yetu kabambe lakini nataka nimhakikishie, maeneo yote ambayo miradi haijakamilika sisi kama Wizara ya Maji na Umwagiliaji tutahakikisha tunaikamilisha ili wananchi wale waweze kufaidika katika suala zima la umwagiliaji.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali, nina swali moja tu la nyongeza. Kwanza nitumie fursa hii kumpongeza sana Waziri wa Elimu, Profesa Ndalichako, Naibu wake na watendaji wote wa Wizara kwa juhudi walizochukua za kuhakikisha kwamba shule hizi za Msakwalo na Farkwa zinapata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni moja tu kwamba katika Shule za Sekondari za Mondo na Soya ambazo nazo ni shule za A-Level zilizopo katika Wilaya ya Chemba, wanafunzi wanatembea umbali mrefu kutafuta maji. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba wanafunzi na walimu wa shule hizi wanapata maji ya uhakika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI, kaka yangu Mheshimiwa Kakunda kwa majibu mazuri, lakini sisi Wizara ya Maji tunatambua umuhimu wa elimu. Kupitia elimu mtoto wa mama ntilie anaweza kuwa Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sisi kama Wizara ya Maji katika bajeti hii tumewatengea Chemba Sh.1,468,000,000. Labda nimuagize Mhandisi wa Maji wa Chemba aone umuhimu sasa kwa shule ambazo ameziorodhesha Mheshimiwa Mbunge wa kuhakikisha wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu yasiyoridhisha kabisa ya Mheshimiwa Waziri ninayo maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, upimaji na uhifadhi wa chanzo cha maji cha Qang’dend si tu ni takwa la kisera na kisheria bali pia ilikuwa ni agizo la Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa alipotembelea bonde la Eyasi mwishoni mwa mwaka 2016. Ni jambo la kushangaza kwa muda huo wote hadi sasa hatua hiyo ya uhifadhi haijafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba, je, Mheshimiwa Waziri, yuko tayari sasa baada ya Bunge hili kwenda kutembelea vyanzo hivyo katika Bonde la Eyasi ili ashuhudie mwenyewe kwamba majibu aliyopewa si sahihi na achukue hatua stahiki kwa hawa ambao wametoa majibu hayo?
Mheshimiwa Naibu Spika, swai la pili; kutokana na mvua nyingi zilizonyesha mwaka huu, chanzo hicho kimeharibika na kuathirika sana kutokana na mchanga kujazwa kwenye macho ya chemchem kiasi kwamba wananchi wenyewe wa Bonde la Eyasi wamejichangisha Sh.21,000,000 na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu kutokana na mapato yake ya ndani imechan gia Sh.35,000,000 ili kuokoa vyanzo hivyo; lakini bado zinahitajika fedha zaidi ili kunusuru vyanzo hivyo. Je, Mheshimiwa Waziri, Wizara yake iko tayari sasa kuweka mkono ili kuunga mkono jitihada za wananchi hao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru, lakini nipende kumjibu Mheshimiwa Mbunge; moja, ukirejea katika majibu ya swali lake la msingi tumeweka alama lakini baadhi ya alama hazionekani. Hata hivyo, kama Naibu Waziri wa Maji nataka nimhakikishie kwamba nipo tayari kufika katika Bonde la Eyasi na kujiridhisha katika haya majibu yametolewa ikitokea kwamba kuna udanganyifu kwa haya majibu, sichelei kusema watapata tabu waliondika haya majibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali lake la pili, ni kuhusu suala zima la sisi kama Wizara kumuunga mkono. Waziri wangu amenipangia kufanya ziara katika mikoa mine, mojawapo ni Mkoa wa Arusha. Nataka nimhakikishie nikifika katika eneo lile Mang’ola nitahakikisha namna gani tunaweza tukashauriana katika kuongeza nguvu zetu ili mwisho wa siku umwagiliaji katika chemchem ile uendelee na wananchi wake waendelee kuzalisha. Ahsante sana.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ambayo yamekuwa yakileta matumaini kwetu na kwa wapiga kura wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niulize swali. Wananchi wa Wilaya ya Nyasa waishio kando kando ya Ziwa Nyasa katika Vijiji vya Mkiri, Ngumbo na Ndumbi wana tatizo la kupata maji safi na salama. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wananchi wale wanapata maji safi na salama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri na nia njema ya wananchi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa sisi kama Wizara yetu ya Maji tulishukuru Bunge lako Tukufu kwa kutuidhinishia fedha kiasi cha Sh.727,345,000,000; na utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Fedha hizi zipo nimwombe Mhandisi wa Maji ajipange sasa katika kuhakikisha wananchi wale wa vijiji ambavyo amevitaja Mheshimiwa Mbunge wanapata maji safi salama na yenye kutosheleza.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa sababu catch line ni kwamba Halmashauri haina uwezo wa kujenga mabwawa, Serikali ipo tayari kutoa pesa hata bwawa moja moja kujenga mabwawa Mkalama katika maeneo yaliyotajwa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa sababu ni ukweli usiopingika kwamba Halmashauri hazina uwezo wa kufanya utafiti, Serikali iko tayari kunipa watafiti nikaondoka nao kwenda kufanya utafiti na mimi nitakuwa nao huko?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyowapigania wananchi wake. Kwa kutambua changamoto kubwa sana ya maji katika Jimbo la Mkalama, Mheshimiwa Waziri wangu aliona haja ya kumsaidia Mheshimiwa Mbunge, akaagiza Mamlaka kwa Wakala wa Uchimbaji Visima (DCCA) kumchimbia visima 20 katika Jimbo lake katika kutatua tatizo la maji. Namwomba Mheshimiwa Mbunge wakati Serikali ikiangalia namna ya kumchimbia mabwawa, asimamie visima hivi ili wananchi wake wapunguze adha ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kumpatia watalaam, sisi kama Wizara ya Maji hatutokuwa na kikwazo chochote kumpatia watalaam aende nao katika kuhakikisha wanafanya utafiti, wananchi wake waendele kupata maji. (Makofi)
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru. Ukiachilia mbali Mkoa wa Kagera uko karibu zaidi na Ziwa Victoria, lakini Mkoa wa Kagera una uhaba mkubwa wa maji. Ni lini sasa Wizara itaamua kubuni mradi mkubwa wa maji kama ule unaotoa maji Ziwa Victoria kwenda Tabora, ukizingatia Mkoa wa Kagera uko karibu zaidi na Ziwa Victoria? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua maji ni uhai nasi kama Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha tunawapatia wananchi maji. Tumefanya jitihada mbalimbali wananchi ambao ni wakazi wanaoishi pembezoni na maziwa kuhakikisha wanapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mkurugenzi wa eneo husika aandae mradi ambao sisi kama Wizara tutaangalia namna ya ku-support kwa haraka wananchi wake waweze kupata maji kwa haraka safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. DKT. IMMACULATA S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Jimbo la Kondoa la Vijijini pia lina uhaba wa mkubwa wa mabwawa na yale yaliyopo yanahitaji ukarabati mkubwa hususan katika bwawa la Kisaki ambalo linahudumia mifugo na wanadamu.
Sasa Serikali ina mpango gani pia wa kuweka jicho la ziada katika Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa Vijijini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu ya Maji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, imekuwa ikichimba mabwawa na hata visima virefu katika maeneo yenye ukame mkubwa sana. Labda nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwa kuendelea kushirikiana na wafadhili wetu, tutaangalia namna ya kuweza kuondoa tatizo hilo na kuwachimbia mabwawa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, Wilaya ya Lushoto ina milima inayotiririsha maji hasa kipindi cha mvua. Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kujenga mabwawa hasa katika maeneo ya Kwekanga, Mbwei, Kwai, Makanya, Bweloi, pamoja na Bonde la Ubiri kwa ajili ya wakulima wa Wilaya ya Lushoto kulima kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge Shekilindi kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini nikubaliane na yeye ipo haja ya Serikali kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha tunafikia azma ya viwanda lazima tuwekeze katika kilimo cha umwagiliaji. Wizara yetu Mheshimiwa Waziri ameona haja sasa ya kupitia mpango kabambe wa mwaka 2002 wa Tume ya Umwagiliaji katika kuhakikisha tunauboresha umwagiliaji ili uweze kuwa na tija na manufaa kwa nchi yetu. Nimhakikishie katika uboreshaji huo watu wa Lushoto hatutawaacha katika kuhakikisha wanawakeza katika kilimo cha umwagiliaji.
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa umaarufu huo wa mabonde katika Ziwa Rukwa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ilishaomba miradi ya umwagiliaji yapata sasa miaka mitano haijapata fedha ambayo ni Maleza, Ilemba, Msiya, Uzia, Kwilo na Milepa. Je, ni lini Serikali itatoa fedha ili miradi hiyo iweze kujengwa kwa manufaa ya wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana. Kikubwa niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge sisi kama Wizara ya Maji kama nilivyoeleza tunaendelea kutokana na changamoto zilizopo katika kilimo cha umwagiliaji ama uwekezaji wa umwagiliaji, tunazo skimu nyingi lakini hazijakamilika, Waziri wangu akaona haja sasa ya kupitia mpango huu kabambe ili tuwe na skimu chache ambazo zitakuwa na tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya mapitio haya katika maeneo ambayo ameyaelekeza tutawekeza fedha katika maeneo yake ili wananchi wanaweza kulima kilimo cha umwagiliaji.
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipatia nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza. Katika majibu yake ya msingi Mheshimiwa Waziri ametamka mradi ambao uko katika Bonde la Ziwa Rukwa lakini uko katika Jimbo langu mradi wa umwagiliaji wa Kirida ambao nilikwishaleta maombi pamoja na mradi wa Mwamapuli. Je, Serikali inakuja na kauli gani sasa kuhusiana na hii miradi ambayo tayari tulikwishawekeza pesa isipokuwa iliharibika kwa ajili ya mvua ili iweze kuendelezwa na kuleta tija kwa wananchi ambao tayari miundombinu ipo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, msimamo wa Serikali ama kauli ya Serikali ni kuhakikisha miradi ya maji ambayo haijakamilika ni kuikamilisha na ile ambayo inahitaji ukarabati tuifanyie ukarabati katika kuhakikisha inaleta tija katika uzalishaji. (Makofi)
MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kuniona. Serikali imejenga miradi ya maji ya Kakonko mjini Gwanu, Mbuki, Dudu A, Nyagwijima, Mamuhange katika Wilaya ya Kakonko. Lakini miradi hii ambayo imetumia takribani shilingi bilioni mbili mingine haifanyikazi hata iliyokamilika haifanyikazi na mingine haijakamilika.

Mheshimiwa Spika, lakini namshukuru Mheshimiwa Waziri Mbarawa amesikia kilio chetu na amekuja, ameikagua miradi hii tarehe 26 Novemba. Sasa kwa kuwa Mheshimiwa Waziri alitoa maelekezo kwa ma-engineer ili wafanye usanifu pamoja na makadirio ya kuikarabati miradi hii kuokoa gharama iliyokwishatumika na akawaelekeza waweke utaratibu wa kubadilisha mfumo wa kusukuma maji kutoka Nishati ya mafuta kwenda nishati ya jua. Je, sasa shughuli hiyo imefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Lakini la pili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wetu Mheshimiwa Mbarawa anafanyakazi kubwa sana na nzuri katika kuhakikisha tunamtua mwanamama ndoo kichwani. Sasa kwa yale ambayo aliyoagiza Mheshimiwa Waziri kwetu ni utekelezaji, tunamuagiza Katibu Mkuu aweze kutatua tatizo hilo kwa haraka ili wananchi wa Kigoma waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza kabisa nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ya kujitosheleza. Naipongeza sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa mradi wa maji wa Wilaya ya Busega, je, mradi huo utaanza lini ili kukidhi mahitaji ya wana Busega?

Swali la pili kwa vile Mkoa wa Simiyu una changamoto kubwa sana ya maji. Je, Naibu Waziri uko tayari kuongozana na mimi baada ya Bunge ukajionee mwenyewe changamoto ya maji ilivyo Mkoa wa Simiyu ili uweze kutatua tatizo hili?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza awali ya yote nimpongeze mama yangu Mheshimiwa Esther Midimu ni miongoni mwa wa mama majasiri na shupavu katika kuhakikisha wanapigania haki za akinamama wakiwemo wamama wa Simiyu.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri Bunge langu halina wamama hili Bunge lina Waheshimiwa tu.

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge, jasiri na mpambanaji katika kuhakikisha anapigania haki za akinamama wakiwemo akinamama wa Simiyu. Nataka nimuhakikishie sisi kama Wizara ya Maji tunatambua kabisa maji ni uhai hatupo tayari kupoteza uhai wana Simiyu tunatarajia mnamo mwezi wa nane mradi huo utaanza na mkandarasi atakuwa site. Lakini suala la kuongozana na mimi kwa kuwa anafanya kazi nzuri nipo tayari kuongozana naye Mheshimiwa Mbunge. Ahsante.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, licha ya Mkoa wa Morogoro kuwa na mito mingi lakini wananchi wa manispaa ya Morogoro hawana maji ya kutosha. Kwa kuwa idadi ya watu katika Manispaa ya Morogoro imeongezeka. Je, Serikali haioni kama kuna umuhimu wa kujenga bwawa lingine lisaidiane na Bwawa la Mindu ili kutosheleza maji kwa wananchi wa Manispaa ya Morogoro?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nikubaliane na dada yangu na Mheshimiwa Mbunge ni ukweli sasa hivi katika mji wa Morogoro watu wameongezeka, uhitaji wa maji umekuwa mkubwa sana. Na sisi kama Wizara tumeona hilo tupo katika harakati katika kuhakikisha tunatafuta fedha ili tuweze kuongeza miundombinu ya maji na wananchi wa Morogoro waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona, labda niseme tu kwamba Mradi wa Maji wa Vijiji Kumi kila Halmashauri kwa upande wetu wa Tanga mradi ule wa Tongoni, Marungu hauna matatizo, lakini mradi wa upande wa Kaskazini kwa maana ya Chongoleani, Kibafuta na Mabokweni kuna tatizo kidogo. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba mradi ule umekuwa ukienda kwa kusuasua, je, ni lini Serikali itafanya utaratibu wa kuhakikisha kwamba mradi ule unawapatia maji wananchi wetu wa vijiji vile nilivyovitaja? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa jukumu la Wizara ya Maji nikuhakikisha wananchi wanapata maji. Mheshimiwa Mbunge amesema Mradi ule wa Chongoleani umekuwa ukienda kwa kusuasua sisi kama Wizara ya Maji hatupo tayari kumuona mkandarasi anafanya kazi kwa kusuasua. Sasa tunamuagiza afanye kazi ili aweze kukamilisha na sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kumpatia fedha kuweza kukamilisha mradi huo. Lakini tukiona anaona hali yake inaendelea kusuasua tutamuondoa tutamuweka mkandarasi ambaye anaweza kukamilisha mradi kwa wakati na wananchi waweze kupata maji.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya majibu ya Serikali, nina maswali ya nyongeza mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kutokana na majibu ya Serikali kuwa Halmashauri ya Iringa na wadau wa maendeleo walichimba visima 53, naomba kujua ni visima vingapi vimetatua matatizo ya maji kwa wananchi wa vijiji hivyo nilivyouliza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa maelezo ya Serikali Mradi wa Maji wa Ibofye utatekelezwa mwaka wa fedha 2019/2020. Mradi huu una miaka 37 umeshindwa kutekelezeka. Naomba kujua ni muujiza gani utakaotumika kwa Serikali kutekeleza mradi ndani wa mwaka mmoja?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kuhusu idadi halisi ya visima ambavyo vipo katika vijiji hivyo alivyovitaja. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge saa saba tukutane ili tuweze kumpa kwa maandishi visima halisi katika vijiji anavyohitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la Mradi wa Ibofye, hii ni Serikali ya Awamu ya Tano, inapoahidi inatekeleza na hata kama haijatekeleza inakuwa na sababu ya msingi na maalum katika suala zima la utekelezaji. Ssisi ni Wizara ya Maji siyo Wizara ya Ukame, tutahakikisha Mradi huu wa Ibofye tunautekeleza ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Spika, nakushuku, kwanza niishukuru Serikali kwa majibu yao katika swali hilo la msingi, lakini nasikitika kwamba maeneo mengi ya Serikali katika majibu haya hayakidhi swali ambalo nimeuliza.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo amesema kwenye jibu la msingi eneo la Mswakini na Makuyuni wanapata maji, lakini tumekuwa tumeleta malalamiko Serikali ya muda mrefu kwamba visima hivyo havitoi maji kwa sababu hakuna nishati ya umeme na Serikali imekuwa ikiahidi kila siku kwamba wanatuletea nishati ya umeme katika visima hivyo. Je, ni lini Serikali itatuwekea umeme katika visima vya Makuyuni na Mswakini ili wananchi wetu waweze kupata maji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nataka commitment ya Serikali kwa kuwa wamesema watatupa fedha kwa ajili ya miradi hii ya maji katika vijiji alivyotaja nini commitment ya Serikali kwamba kwa mwaka wa fedha 2019/2020 tutapata fedha ya kutosha kwenye Bajeti kwa ajili ya miradi hii ambayo usanifu wake umekamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Kalanga kwa kazi nzuri ambayo anaifanya katika Jimbo lake la Monduli na nimeshakwishafika Monduli tumeona kazi kubwa anayoifanya na sisi kama Wizara ya Maji tutahakikisha tunamuungisha mkono katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Lakini kuhusu suala zima la nishati ya umeme nataka nimuhakikishie tutafanya mawasiliano ya haraka na watu wa Wizara ya Nishati katika kuhakikisha eneo la Makuyuni wanapatiwa umeme ili uendeshaji wake uwe wa nafuu na wananchi waweze kupata maji.

Mheshimiwa Spika, lakini suala zima la bajeti la mwaka 2019/2020 tunakumbuka Mheshimiwa Kalanga mbele ya Mheshimiwa Rais katika wakati anaweka jiwe la msingi katika mradi wa maji Arusha ulitoa malalamiko yako na ukaomba atakapotembea na kudhulu wengine asikupite. Sisi kama Wizara ya Maji hatutokupita wala hatutokuacha wala hatutokutosa katika kuhakikisha tunakuongezea bajeti na wananchi wako waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.
MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi pamoja na majibu ambayo yametolewa na Serikali niishukuru kwamba Serikali imekuwa ikiongeza bajeti tulikuwa shilingi milioni 500, shilingi milioni 800 na mmefika shilingi bilioni 1.4. Lakini swali la msingi lilikuwa ni kwamba tunapandisha vipi kiwango ha upatikanaji maji safi na salama kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo na tupate angalau bilioni tatu.

Sasa je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuwa na mjadala na Mbunge pamoja na watendaji wake wa Wizara ili kuona namna gani kiwango kinaongezeka kutoka shilingi bulioni 1.4 angalau tuwe na reasonable amount ambayo itaweza kutatua changamoto hii?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya. Lakini kikubwa tunatambua kabisa maji ni uhai na jukumu la Wizara yetu ya Maji ni kuhakikisha watanzania na wana Nsimbo wanapata maji safi, salama na yenye kutosheleza. Sasa katika kuhakikisha tunalinda uhai wa wana Nsimbo sisi kama Wizara ya Maji tupo tayari kufanya mjadala na Mheshimiwa Mbunge nadhani baada ya Bunge hili tukutane tuweze kukutana na watendaji wetu ili tuweze kujadiliana ni namnaa gani tunaweza tukatatua tatizo la mji Nsimbo kwa haraka. Ahsante sana.
MHE. DKT. TULIA ACKSON: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, changamoto zilizopo Wilaya Mbarali zipo pia Wilaya ya Rungwe hususani kwenye eneo la Bonde la Mwakaleli lakini pia Kata ya Ikuti. Maeneo haya yanazungukwa na mito lakini hayana miundombinu ya kupelekea wananchi maji. Nataka kujua ni lini Serikali itapekeza miradi ili wananchi waweze kupata maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, changamoto hizi pia zipo kwenye kata mbalimbali ya Mbeya Jiji. Baadhi ya kata hizo zenye changamoto ni pamoja na Kata ya Mwasekwa, Mtaa wa Ilembo na Mengo; Kata ya Iganjo, Mtaa Mayombo na Rumbila; Kata ya Iduda, Mtaa wa Muhala; Kata ya Uyolem, Mtaa wa Hasanga; Kata ya Msalaga, Mtaa wa Ntundu na Itezi Mashariki; Kata Iwambi, Mtaa Mayombo na Lumbila, Itagano kwenye mtaa mingi, Itenda baadhi ya mitaa. Nataka kujua ni lini Serikali itapeleka maji kwa wananchi Kata hizi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda tutambue kwamba maji ni uhai. Nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Naibu Spika kwa kutetea uhai wa wananchi wa Mbeya. Kama Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha Watanzania wakiwemo wananchi wa Mbeya wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu la Bonde la Mwakaleli tuna mradi pale wa zaidi ya shilingi bilioni 6 ambao utaweza kunufaisha wananchi wa Kata ya Masebe pamoja na Suma. Kwa Kata ya Ikuti katika Jimbo lile la Rungwe, tunamuagiza Mhandisi wa Maji wa Wilaya ya Rungwe afanye usanifu haraka ili wananchi wale waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la Jiji la Mbeya, uzalishaji wa Mamlaka ya Maji ya Mbeya ni lita milioni 48, 45 kwa siku. Mkakati wa muda mfupi ni kuhakisha tunatumia miundombinu ya sasa iliyopo ili wananchi wa Iwambi, Iganzo, Iduda, Itende, Uyole na Isesya nao wanapata maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Naibu Spika hata maeneo yenye miinuko kwa maana Mwansekwa pamoja na Itagano nao tutawapelekea maji kwa sababu sisi siyo Wizara ya ukame. Kwa hiyo, nataka nimhakikshie Mheshimiwa Naibu Spika sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wa Jiji la Mbeya kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Kijiji cha Kipangege, Kata ya Soga mradi wa maji tayari umeshakamilika lakini hadi hivi sasa wananchi hawajaanza kutumia maji hayo. Je, lini sasa mradi huu utakamilika na kuanza kutoa maji ili wananchi wa Kata ya Soga waanze kufurahia huduma ya maji safi na salama?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tatizo hili pia linafanana na tatizo la Wilaya ya Arumeru katika Jimbo la Arumeru Magharibi, Kata ya Bwawani ambapo mradi wa maji tangu enzi za aliyekuwa Mbunge Elisa Mollel na Ole- Medeye ulianza kujengwa mpaka leo hii bado haujakamilika na Serikali imekwishatoa fedha mkandarasi hayupo. Napenda tu kufahamu majibu kutoka kwa Serikali, nisikie kauli yao juu ya mradi huu ili wananchi wa Kata ya Bwawani nao waweze kupata maji na kuondokana na changamoto kubwa iliyopo hivi sasa. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma kwa kazi nzuri anayoifanya katika Mkoa wa Pwani. Kikubwa sisi kama Wizara ya maji jukumu letu ni kuhakikisha Wanapwani, kwa maana ya Soga, waweze kupata maji safi na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, amesema katika Kijiji kile cha Kipagenge katika Kata ya Soga kuna mradi lakini wananchi hawapati maji. Nataka nimhakikishie baada ya Bunge nitafanya ziara katika eneo hilo la Soga, niangalie ili mwisho wa siku mradi ule uweze kukamilika na wananchi waweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia dada yangu Amina Mollel amezungumza kwamba sasa mradi umekuwa wa muda mrefu sana, kwamba Serikali imekwishatoa fedha lakini mkandarasi hayupo site. Nimhakikishie katika maeneo nitakayotembelea basi na Arumeru Mashariki nitafika na kuhakikisha tunaongeza nguvu katika mradi ule ili wananchi waweze kupata maji safi na salama na yenye kutosheleza.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Tatizo la Pwani linafanana kabisa na tatizo lilipo Wilaya ya Magu katika miradi inayoendelea Sola, Kisamba, Bubinza, Matelamuda, pamoja na Kabila Ndagalu na Kitongo Sima, miradi hii imesimama sasa kwa sababu wakandarasi wamesha-raise certificate na Wizara tayari inazo taarifa hizo. Je, ni lini Wizara italipa fedha kwa wakandarasi ili miradi hiyo iweze kuendelea?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Kiswaga kwa kazi nzuri sana anayoifanya katika Jimbo lake la Magu. Tunatambua kwamba utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha. Sasa sisi kama viongozi wa Wizara hatutakuwa kikwazo katika kuwapatia wakandarasi wake fedha. Nimwombe baada ya Bunge tukutane ili tupate zile certificate tuangalie namna bora ya kuwapatia fedha ili wakandarasi waendelee na kazi.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Waziri siku za karibuni alitembelea Rombo na walimtembeza kwenye miradi ya Leto, Ngareni na Shimbi Mashariki. Hii ni miradi ambayo ilikuwa katika ile miradi ya World Bank ya visima 10 na ni ya siku nyingi na imeshakamilika; na kila Waziri anapokuja Rombo hapelekwi kwenye miradi mingine ni hiyo mitatu tu. Je, Mheshimiwa Waziri sasa yuko tayari kuiagiza halmashauri, maji ambayo yameshapatikana wagawiwe wananchi badala ya kufanya siasa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipende kumjibu mzee wangu hapa; kwamba sisi kama viongozi wa Wizara tunapotoa huduma ya maji tunalinda uhai wa Watanzania na tunapeleka huduma hii kwa wana-CCM na hata Wana- UKAWA. Nataka nimuhakikishie kwa kutibitisha hilo, kwamba hata katika certificate tulizozilipa mwaka huu katika mwezi huu zaidi ya milioni 20 tumepeleka katika jimbo lake. Sasa nataka niwaambie wataalam wetu wa Wizara ya Maji, wahakikishe wanapeleka huduma hii muhimu kwa Wanarombo. Ahsante sana.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Halmashauri ya Lindi Vijijini na hasa Jimbo la Mtama tulipanga mwaka huu wa fedha kuchimba visima virefu 25 na fedha zipo, tumeomba kibali toka kibali toka mwezi wa Nane mwaka jana, tukaandika barua kukumbusha mwezi wa Kumi na Mbili lakini mpaka sasa hatujibiwi chochote, tatizo la vibali hivi ni nini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mbunge, Mheshimiwa Nape, nimefanya ziara katika Jimbo la Mtama, ni mmoja kati ya Waheshimiwa Wabunge wanaofanya kazi nzuri sana katika majimbo yao. Sisi kama Wizara ya Maji hatuko tayari kukwamisha jitihada anazozifanya. Nimwombe tu baada ya Bunge tuweze kukutana na Katibu Mkuu ili tuweze kupata vibali hivyo ili wananchi wake waweze kupata huduma ya msingi.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyonge. Pamoja na kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri sana iliyofanya ya kujenga miundombinu katika Mji wa Musoma kiasi kwamba maji sasa hivi yanapasua mpaka mabomba na maji yanayozalishwa kwa saa ni takribani lita elfu 12, lakini maji yale yanaweza kupelekwa mpaka Wilaya ya Butiama, Kata za Bukaga, Mkanga, Makatende mpaka Bisuma. Vile vile maji haya yanaweza kufika mpaka Jimbo la Musoma Vijijini katika Kata za Etalo, Nyakatende, Nyigima pamoja na Nyamimange. Ningependa kujua, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo ambako chanzo cha maji yaliyoleta maji ya Musoma wanaweza kupata na wenyewe huduma ya maji safi na salama kutokana na chanzo hicho cha maji? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Makilagi kwa kazi nzuri ya kuwatetea Wanamara, lakini kikubwa Serikali imefanya kazi kubwa sana ya kuwekeza mradi zaidi ya bilioni 45 pale Musoma. Kwa hiyo changamoto kubwa ni suala zima la usambazaji, sisi hilo tumeliona na tutahakikisha tunawekeza fedha ili tusambaze maji ili maeneo hayo aliyoyataja yaweze kupata maji safi salama na yenye kutosheleza.
MHE. AMINA N. MAKILLAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri na pamoja na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana inayoifanya ya kujenga miundombinu ya maji, kiasi cha kufikia kiwango cha asilimia 80 mijini na asilimia 64.8 vijijini, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Kwa sababu Mkoa wa Mara ni Mkoa ambao umezungukwa na Ziwa Victoria na una Mto Mara, Mto Robana, Mto Simiyu na Mto Suguti; lakini Mkoa wa Mara bado ipo changamoto kubwa ya upatikanaji wa majisafi na salama, kwa upande wa vijijini ni asilimia 50.7 na mijini ni asilimia 60. (Makofi)

MWENYEKITI: Swali.

MHE. AMINA N. MAKILLAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Mkoa wa Mara ambao unazungukwa na Mito na Miji unapelekewa maji safi na salama na kufikia kiwango ambacho kimetajwa kwenye Ilani ya CCM?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa kuna kazi nzuri sana inayofanywa na Serikali ya kutafuta fedha na kuwalipa Makandarasi wa miradi ya maji, lakini kwa Mkoa wa Mara tunalo tatizo kubwa sana. Kuna tatizo la kutolipa Wakandarasi. Wilaya ya Serengeti kuna miradi miwili, milioni 500 tayari wamesha-raise certificate hawajalipwa; Musoma Vijijini miradi mitatu, tumesha-raise certificate bilioni 1.6 hawajalipwa, Serengeti tuna miradi mitatu, shilingi milioni 500 haijalipwa na hata Butiama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha, kwa kuwa tumeshapeleka certificate, Wakandarasi waweze kulipwa fedha na miradi iweze kuendelea kwa sababu miradi yote imesimama na sasa ni mwezi wa nne? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimpongeze Mheshimiwa Amina Makillgi, amekuwa ni mtetezi mkubwa sana hususan suala linalohusu haki za huduma ya jamii ikiwemo katika suala zima la maji. Sisi kama Wizara Maji ni jukumu letu kuhakikisha Watanzania wakiwemo wana Mara wanapata majisafi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji, Serikali imefanya jitihada kubwa sana. Ukienda Musoma, zaidi ya shilingi bilioni 45 za mradi mkubwa tumewekeza, kazi iliyobaki ni kwenda kusambaza maeneo ambayo hayana maji wapate maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati uliopo sasa hivi, tuna miradi zaidi ya 26 ambayo hivi karibuni tunataka tuitekeleze. Tupo katika hatua ya utangazaji wa tender kwa maana ya manunuzi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika miji 26 kupitia fedha za India, dollar takribani zaidi ya milioni 500 katika miji ya Tarime pamoja na Mgumu kwa kaka yangu Mheshimiwa Ryoba nao watapatiwa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tupo katika hatua za mwisho sasa za kumpata Mkandarasi katika kuhakikisha tunaanzisha mradi ule mkubwa wa Mgango – Kyabakari mpaka Butiama katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji kwa Mheshimiwa Muhongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa na cha msingi kabisa kuhusu suala zima la kuwalipa Wakandarasi, sisi kama Wizara ya Maji, wapo baadhi ya Wakandarasi wanafanya kazi nzuri. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha Wakandarasi wote waliofanya kazi nzuri za kutekeleza miradi ya maji, tutawalipa kwa wakati, lakini kwa wale wababaishaji, lazima tuwashughulie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa namwomba Mheshimiwa Makilagi tukutane baada ya saa 7.00 tuone certificate zake na tuweze kujiridhisha ili tuweze kuwalipa Wakandarasi wake na wananchi wake wa Mara weweze kupata majisafi na salama na yenye kutosheleza. (Makofi)
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa muda wa kuuliza swali la nyongeza. Napenda kuishukuru Wizara kwa kutuchimbia visima 14, kilichobaki ni ujenzi na uwekaji wa pump.

Je, ni lini fedha za kumalizia ufungaji wa pump zitaletwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nampongeza Mheshimiwa Kapufi kwa jitihada zake kubwa za kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. Alishakuja Wizarani siyo mara moja wala mara mbili katika kuhakikisha wananchi wake wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na uwepo wa chanzo. Tumeshachimba visima vya kutosha. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Kapufi, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika utoaji wa fedha ili wananchi wale waweze kutengenezewa miundombinu na waweze kupata majisafi na salama. (Makofi)
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Naomba kuuliza swali la nyongeza. Mji mdogo Mwandiga ni moja ya eneo ambalo linakabiliwa sana na changamoto ya kukosa majisafi na salama. Ni lini sasa Serikali itatimiza ahadi yenu ya kuleta maji ya Manispaa ya Kigoma Ujiji na kufika katika mji mdogo wa Mwandiga?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika Mkoa wa Kigoma una jitihada kubwa sana kwa Manispaa ile ya kutekeleza mradi wa zaidi ya Euro milioni 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukamilishaji wa mradi huu, sisi kama Wizara ya Maji, tutahakikisha kupeleka maji katika Mji wa Mwandiga. Nataka nimhakikishie ndugu yangu, safari moja huanzisha nyingine. Acha tukamilishe safari hii, lakini safari nyingine tutakamilisha katika kuhakikisha tunapeleka maji Mwandiga.
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa. Mradi wa Maji kati ya Kisiwa cha Jibondo ambao una thamani ya zaidi ya shilingi bilioni mbili, Mkandarasi ameshaujenga na sasa amefikia asilimia zaidi ya 70. Mradi unatakiwa ukabidhiwe mwezi Machi mwaka huu. Mpaka sasa Mkandarasi hajalipwa hata senti tano na certificate zipo Wizaran. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza akatuhakikishia ni lini sasa Mkandarasi huyo atalipwa ili aweze kumaliza mradi ule?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nampongeza Mheshimiwa Dau kwa kazi nzuri sana anayofanya kwa wananchi wake wa Mafia na pamoja na Jibondo. Tunatambua kabisa wananchi wa Jibondo wamekuwa na changamoto kubwa sana katika suala zima la maji na hata chanzo cha maji kukosekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara tumeona haja sasa ya kutekeleza mradi mkubwa na tunatambua kazi nzuri aliyoifanya Mkandarasi. Nataka nimhakikishie, katika mgao wa mwezi huu Mheshimiwa Mbarawa ameshatenga fedha zaidi ya shilingi milioni 200 katika kuhakikisha tunamlipa Mkandarasi yule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwaagiza Mhandisi wa Maji wa Mafia, fedha zile zitakapofika ahakikishe anamlipa Mkandarasi haraka ili asimkwamishe katika suala zima la utekelezaji na wananchi waweze kupata maji. (Makofi)
MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru. Kwa kuwa Mji wa Kisesa kulikuwa na mpango wa kuwekwa maji ya bomba pamoja na Vijiji vya Mahaha, Kabila, Dagalu huko. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwafikishia maji wananchi hawa ili waweze kupata huduma hiyo inayostahili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa na jitihada kubwa sana katika Mkoa wa Mwanza katika kutatua tatizo la maji. Kuna utekelezaji wa miradi mikubwa sana Magu, Lamadi pamoja na maeneo mengine. Nataka nimhakikishie; nami kama Naibu Waziri, baada ya Bunge nataka nifike katika Jimbo lake ili twende tuka-push miradi ile iweze kukamilika na wananchi wake waweze kupata maji.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kifupi sana. Kwa kuwa Serikali kupitia Hazina ilitenga shilingi bilioni 299.9 katika bajeti yake ya mwaka huu wa fedha na mpaka sasa wametoa shilingi bilioni 1.67 sawa sawa na 0.6; na maji bila fedha ni sawa sawa na hakuna kitu. Kwa hiyo swali langu ni dogo; ipi ni commitment ya Serikali kwamba watatoa hizo fedha kabla ya mwaka huu wa fedha kwisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua sisi kama Serikali kwamba maji ni uhai na utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha, lakini Serikali imekuwa na vyanzo mbalimbali katika kuhakikisha tunatatua matatizo ya maji.

Moja, tuna Mfuko wa Maji, Bunge lako Tukufu limeidhinisha kiasi cha shilingi bilioni 158. Nataka nimhakikishie kwamba mpaka sasa zaidi ya shilingi bilioni 80, tumeshazipata katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, hii ni Serikali ya Awamu ya Tano, tunaahidi, tunatekeleza katika kuhakikisha tunamtua mwanamama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niulize swali la nyongeza. Dhamira njema ya Serikali imeleta mradi mkubwa wa kusambaza maji katika Mji wa Itigi. Wakandarasi walipewa ruhusa ya kuanza mradi ule bila pesa. Je, Serikali iko tayari sasa kuwalipa certificate zao ambazo tayari wamesha-raise katika Wilaya hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya, lakini tunatambua maeneo ya Itigi ni moja ya maeneo yenye changamoto kubwa sana ya maji. Nasi kama Wizara ya Maji tukaona haja sasa ya kuutekeleza mradi ili wananchi waweze kupata maji. Sisi kama Wizara hatutakuwa kikwazo kwa Wakandarasi wenye uwezo na wenye sifa na wanaotekeleza kazi zao vizuri kuwalipa kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutamlipa certificate yake ili Wakandarasi waendelee na kazi.
MHE. DKT. TULIA ACKSON: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, yanayoonesha kwamba sasa Vijiji vya Ibungila na Lubiga vitapata maji kupitia mradi huu, upo mradi wa Masoko Group ambao umesuasua kwa muda mrefu, naomba Mheshimiwa Naibu Waziri atuambie ni lini mradi huu utakamilika ili wananchi wa vijiji vya Kata ya Masoko waweze kupata maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, uchakavu wa miundombinu katika Kata mbalimbali za Mbeya Jiji hususan Kata ya Ilomba, Mtaa wa Hayanga – Ituha, Tonya na Ihanda, Kata ya Iganzo Mtaa wa Igodima na Mwambenja, Kata ya Iyunga Mtaa wa Sistila, Kata ya Ghana Mtaa wa Magharibi na Mashariki, Iganjo Mtaa wa Iganga na Igawilo Mtaa wa Sokoni na Chemi: Ni lini Kata hizi zitapelekewa miradi ili ziweze kupata maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, Dkt. Tulia kwa kazi nzuri sana anayoifanya na katika kuhakikisha anawatetea wananchi waweze kupata maji. Kubwa sana ni kuhusu suala zima la kusuasua kwa mradi wa maji wa Masoko Group.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge, nilifanya ziara katika eneo lile la Masoko Group na tukaona usuaji wa mradi ule, tukaagiza timu ya Wizara ili iweze kufika na kuongeza nguvu katika kuhakikisha mradi ule unakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Naibu Katibu Mkuu Engineer Kalebelo, alifika na timu ya Wizara pale na wakazungumza na Mkandarasi na wakampa mikakati mpaka sasa asilimia 60 ya mradi umeshakamilika na wananchi wa Mpera gwasi na Nsanga sasa hivi wanapata maji safi na salama na ya kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji tutahakikisha tunausimamia mradi ule kwa dhati kabisa ili uweze kukamilika na vijiji takribani 15 vilivyopangwa kunufaika, viweze kunufaika na mradi wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, Mheshimiwa Mbunge hii ni wiki ya pili ananiulizia swali la maji katika Jiji la Mbeya. Nataka nikuhakikishie, ukimwona mtu mzima analia, ujue kuna jambo. Hivyo, katika wiki ya kwanza tuna maswali mawili katika Jiji la Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, nipo tayari sasa kukutana na wataalam wetu wa Jiji la Mbeya kwa maana ya Majisafi na Usafi wa Mazingira katika Jiji la Mbeya ili tujipange ni namna gani tunaweza tukapeleka maji kwa haraka katika maeneo ambayo ameyasema ya Ilomba, Iganzo, Iyumba, Ghana na Iganjwa.
MHE. HUSSEIN M. BASHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na kuishukuru Serikali kwa mradi wa maji wa Ziwa Victoria na mradi wa visima 25 katika Jimbo la Nzega, sasa nilitaka nimwombe Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kutupatia commitment Halmashauri ya Mji wa Nzega kupatiwa fedha kiasi cha shilingi bilioni 1.2 katika mwaka wa fedha unaokuja ili kukamilisha mradi wa maji katika Vijiji vya Mhogola, Monyagula, Migua, Itangili, Igilali, Mwanzoli na Kitengwe?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kifupi kwanza, nimpongeze Mbunge, kaka yangu Mheshimiwa Hussein Bashe, kwa kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo lake la Nzega, lakini kubwa tunatambua utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha, nimwombe basi tukutane mimi na yeye, pamoja na Wataalam wetu wa Wizara, tuangalie namna gani tunaweza tukasaidiana. Ahsante sana.
MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nini sasa commitment ya Serikali? Financing agreement ni lini itasainiwa ili miji hii midogo iweze kupata maji?

Swali la pili, kwa kuwa kuna mradi ambao ulikuwa umeanza upembuzi yakinifu na umeshakamilika katika Ziwa Victoria ambao utanufaisha Wilaya ya Kwimba Jimbo la Sungwe na Wilaya ya Maswa Jimbo la Malampaka na Vijiji vya Magu takribani 40, ni lini mradi huo utaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Magu kwa kazi nzuri sana na kuweza kuwapigania wananchi wake mpaka ule mradi wa Euro milioni 104 kuweza kuanza katika Jimbo lake. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba safari moja huanzisha nyingine. Tunatekeleza mradi huu, lakini kwa kuwa ile ni kazi ya nyongeza, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo, tutafanya mawasiliano haraka, pamoja na wenzetu wa Wizara ya Fedha ambao wamekuwa na mchango mkubwa katika Wizara yetu; tutashirikiana kwa haraka ili mradi huu uweze kusainiwa na uweze kupeleka maji katika eneo lake.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala zima la eneo lake kwa vijiji alivyovitaja pamoja na suala la upatikanaji wa maji, maeneo mengi ya Magu pamoja na Sumve yamekuwa karibu sana na Ziwa Victoria. Siyo busara sana kuona tuna rasilimali hizi za kutosha halafu maji yale yasinufaishe wananchi. Sisi kama Wizara ya Maji, tuna Mhandisi Mshauri sasa hivi anayefanya kazi ya upembuzi katika kuhakikisha rasilimali ile ya Ziwa Victoria, maeneo ya miji yaliyoko karibu waweze kupata maji safi na salama yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Sumve pamoja na Mheshimiwa wa Magu, sisi kama Wizara ya Maji, tumejipanga katika kuhakikisha mradi ule utakapokuwa umeshasanifiwa, utaanza kwa haraka ili wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nami napenda kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa mradi unaotegemewa kutekelezwa pale Magu unategemea sana chanzo kipya kitakachojengwa kwenye Jimbo la Nyamagana pale Butimba ambao utasaidia pia maji kule Buswelu kwenye Jimbo la Ilemela, ikiwemo Kata ya Buhongwa kama ilivyotajwa, Kishili, Rwanima pamoja na Igoma.

Mheshimiwa Spika, mradi huu tayari mkandarasi wa kusambaza bomba za maji ameshapatikana na mkandarasi wa kujenga chanzo hiki kipya ndio imekuwa inasuasua. Mheshimiwa Kiswaga ameomba commitment ya Serikali, sasa Mheshimiwa Waziri atuhakikishie kwamba hii financial agreement ni lini itakuwa tayari ili miradi hii iweze kutekelezeka kulingana na hali halisi ilivyo?

Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa maji na uwepo wa Ziwa Victoria haufurahishi leo watu wa Mwanza, Nyamagana pamoja na miji inayozunguka kuendelea kuchota maji kwenye visima.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nampongeza kaka yangu Mheshimiwa Mabula kwa kazi nzuri anayoifanya katika Jimbo lake la Nyamagana, lakini atambue kabisa eneo ambalo litapata maji kwa asilimia 100 ni eneo la Nyamagana. Sasa sisi kama Wizara kuna kazi kubwa sana inayofanyika, hiki kilichobaki ni kiasi kidogo sana.

Mheshimiwa Spika, kubwa, nataka nitengeneze commitment kwake kwamba sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji na siyo Wizara ya Ukame tutafanya mawasiliano ya haraka na Wizara ya Fedha kuona ule mkataba unasainiwa kwa haraka ili mwisho wa siku mkandarasi yule aweze kuhakikisha chanzo kile cha maji kinatekelezwa kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa miradi mingi ya maji imesimama katika Wilaya ya Mpwapwa na Kongwa na hivi sasa wananchi wanakosa huduma ya maji; makandarasi hawajalipwa fedha:-

Je, Mheshimiwa Waziri anasemaje kuhusu hili? Ni lini makandarasi watalipwa miradi ikamilike na wananchi waweze kupata maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ukimwona mtu mzima analia ujue kuna jambo. Nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Kiukweli tulikuwa na madai ya makandarasi takribani zaidi ya shilingi bilioni 104.5. Tunashukuru sana Wizara ya Fedha, baada ya kufanya ukaguzi imeonekana makandarasi ambao wanatakiwa kulipwa, wanadai zaidi ya shilingi bilioni 88. Wameshatupa fedha zaidi ya shilingi bilioni 44 mwezi huu Machi na wametupa commitment ndani ya mwezi huu wa Nne watatupa tena shilingi bilioni 44 katika kuhakikisha makandarasi wote fedha zao zinalipwa.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama kuna certificate yake hajalipwa, tuwasiliane tumlipe. Nataka nimhakikishie, baada ya kumlipa, ataendelea kuwa juu juu kileleni katika Jimbo lake la Mpwapwa. Ahsante sana.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mheshimiwa Naibu Waziri nakushukuru sana kwa majibu mazuri. Kwa kweli hicho ni kilio cha muda mrefu kwa wananchi kuhusu bili na kuhusu upatikanaji wa hizi pre-paid meters.

Mheshimiwa Spika, katika jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Serikali imeagiza Mamlaka zote nchini kuendelea kuwafungia wananchi; swali langu ni kwamba: Je, ni lini sasa wamewaagiza muda wa kumaliza kufunga hizi meters? Maana isije ikachukua muda mrefu, tuweze kuwapunguzia adha hii ya bili kubwa na wananchi waweze kupata maji kwa bili ambayo ni ya uhakika.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, hii ni changamoto, lakini sisi kama Wizara tumeliona. Nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuwatetea wananchi wake wa Morogoro pamoja na Watanzania kwa ujumla kutokana na changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza tumewaita Wakurugenzi wote katika Wizara yetu kwa maana ya Mamlaka za Maji na Mheshimiwa Waziri akawapa agizo hili kutokana na changamoto hii. Kikubwa, sisi katika kuhakikisha tunaongeza utendaji, tumewasainisha mikataba (performance agreement) kwa maana ya utendaji wao. Huwezi ukawa Mkurugenzi wa Maji halafu kumekuwa na changamoto katika suala zima la upatikanaji wa maji. Kwa hiyo, ninachotaka nimhakikishie, sisi kama viongozi wa Wizara tutawapima kwa yale maagizo tuliyowapa kuhakikisha wanatekeleza kwa wakati ili kuweza kuondoa changamoto hizi za bei pamoja na maeneo mengine ambayo hayajafikiwa na usambazaji wa maji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa tena nafasi. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza ikiwemo kushukuru ziara ya Makamu wa Rais ambaye alibaini ubadhirifu wa mradi wa Nyahaa, natumaini Wizara inaendelea kulifanyia kazi suala hilo. Swali la kwanza, je, Serikali iko tayari kuongeza fedha za utafiti hususan katika maeneo yasiyo na miradi mikubwa kama ile iliyopitiwa na maji ya Ziwa Victoria au mkopo wa India ikiwemo Mkalama ili kuweza kupata vyanzo vya uhakika vya maji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili je, ni kweli Serikali inatekeleza miradi hiyo na pesa hizo zilitengwa, je ni lini certificate za wakandarasi zitalipwa ili kazi iweze kuendelea kwa sababu kazi kule imesimama kutokana na wakandarasi kutokulipwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Allan Kiula Mbunge wa Jimbo la Mkalama kwa kazi nzuri sana anayoifanya katika jimbo lake. Kubwa ni kuhusu suala zima la utafiti, sisi kama Serikali tunautambua umuhimu wa suala zima la utafiti hasa katika sekta ya maji kwa sababu italeta mapinduzi makubwa. Nataka nimhakikishie sisi kama Serikali hatutokuwa kikwazo kuongeza fedha za utafiti kadiri bajeti itakavyokuwa imeruhusu katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na tafiti ambazo zitaruhusu kufanya mapinduzi katika sekta ya maji.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu suala zima la madai ya wakandarasi hususan katika miradi ya jimbo lake. Utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, tukubali tulikuwa na madai zaidi ya bilioni 88 ya wakandarasi lakini tunashukuru Wizara ya Fedha ijumaa imetupa zaidi ya bilioni 44 kwa ajili ya kuwalipa wakandarasi certificate zao na wametupa commitment ndani ya mwezi huu wa nne watatupa bilioni 44 zingine kwa ajili ya kuwalipa wakandarasi fedha zao.

Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge apate nafasi ya kuwasiliana na sisi katika kuhakikisha tunamlipa mkandarasi wake ili aweze kuendeleza miradi ya maji katika Jimbo lake la Mkalama.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza niishukuru Serikali kwa hatua ambayo imefikia kwenye usanifu, lakini niombe kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa sababu ya hali ngumu kwa wananchi wa Jimbo la Kyerwa hasa hasa kwenye vijiji ambavyo vinaguswa na mradi huu, je, Serikali iko tayari kwenye bajeti ya 2019/2020 kutenga angalau kiasi kidogo ili mradi huu uweze kuanza wakati Serikali inaendelea kutafuta hela kubwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuna miradi ambayo iko katika Kata ya Mabira, Lukulaijo na kwenye Kijiji cha Kageni miradi hii imeshaanza lakini wakandarasi wamekuwa wakienda kwa kusuasua kwa sababu bado certificate zao hazijalipwa. Je, Serikali iko tayari kuwalipa wakandarasi hawa ili waweze kukamilisha hii miradi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Bilakwate, mimi binafsi nilipata nafasi ya kwenda katika jimbo lake, nimeona kazi kubwa anayoifanya katika jimbo lake pamoja na wananchi wake. Sasa nataka nimhakikishie sisi kama Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo kwa wananchi wa Kyerwa kupata maji safi salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Spika, tumefanya tathmini ule mradi ni fedha nyingi sana, lakini tunatambua maji ni uhai na hayana mbadala. Sasa nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ukikosa ziwa la mama, la ngombe unanyonya, sisi tupo tayari kufanya njia mbadala katika kuhakikisha wananchi wake wa Kyerwa wanapata maji safi na salama ili waweze kuishi katika eneo lake. Kikubwa na cha msingi kabisa nimwombe kutokana na kuna miradi ambayo inaendelea katika jimbo lake, tukutane baada ya saa saba ili tuangalie ni namna gani tunamsaidia katika kuhakikisha fedha zile tunazilipa wananchi wake waweze kupata maji safi.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nashukuru sana kwa majibu ya Naibu Waziri, ni kweli muda mfupi umeanza ambao ni mzuri sana, ambao wanaweza wakatoa maji kwenye kata mbalimbali, lakini kuna Kata ya Magadu ambao waliahidiwa maji, ambao hakuna maji kabisa na ilikuwa wachimbiwe kisima cha muda mfupi angalau waweze kupata maji, lakini mpaka sasa hivi Kata ya Magadu wana shida sana ya maji. Je, ni lini wataweza kupatiwa hicho kisima au kuchimbiwa maji wakaweza wakapata maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, mradi huu ambao unafadhiliwa kwa Euro milioni 70 umechukua muda mrefu na tukiwa tunasubiri kwa muda mrefu wa miaka zaidi ya mitatu sasa tunaambiwa kuwa imebaki kusainiwa; je, kwa sababu wananchi wa Morogoro Manispaa wanategemea maji yao kutoka bwawa la Mindu, kuna mkakati gani wa muda mfupi ambao Serikali inaweza ikafanya kukarabati bwawa la Mindu?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, mama yangu, Mheshimiwa Christine Ishengoma, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kuhakikisha anawasemea wananchi wake wa Mkoa wa Morogoro. Kubwa ni kuhusu suala zima la maji katika Kata ya Magadu. Nimuagize tu Mhandisi wa Maji wa Mkoa, sisi ni Wizara ya Maji, siyo Wizara ya ukame, ahakikishe anasimamia suala hili la uchimbaji wa kisima wananchi wa Magadu waweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la mradi huu mkubwa wa Euro milioni 70. Tunapozungumzia maji, ni rasilimali muhimu sana, lakini sasa hivi Morogoro kumekuwa na uhitaji mkubwa sana, uzalishaji wetu sisi ni lita milioni 30 lakini kutokana na ongezeko la watu pamoja na taasisi na viwanda, kumekuwa na uhitaji wa zaidi ya lita milioni 59 na ndiyo maana sisi kama Serikali tukaona haja sasa ya kuwekeza kwa maana ya kuongeza bwawa la Mindu, katika kuhakikisha kwamba linakuwa na uzalishaji mkubwa ili wananchi wa Morogoro waweze kupata maji safi, salama na kuweza kukuza uchumi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kilio hiki cha muda mrefu, lakini kubwa nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, kwa hiyo, pamoja na utoaji huu wa fedha lazima tufuate utaratibu. Nataka nimtie moyo kwamba wawe na subira, subira yavuta heri na heri itapatikana katika upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Jimbo la Rombo lina shida kubwa sana ya maji, pamoja na hayo Serikali ina jitihada inazofanya kama za kupata maji katika Ziwa Chala, kupanua lile bomba kubwa linalotoa maji Marangu kuleta Rombo na kadhalika. Hata hivyo, shida hii inakuzwa sana na jinsi KILIWATER (Taasisi ya Wananchi) inavyogawa maji kule Rombo, inagawa kwa upendeleo, inagawa kwa baadhi ya watu, haifungii watu mita na kadhalika. Baraza la Madiwani…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Selasini uliza swali tafadhali.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Sasa kwa kuwa tulishaazimia taasisi hii iondolewe na Serikali ilishakubali; je, Mheshimiwa Naibu Waziri, yuko tayari kwa muda wake twende Rombo ili akakague shughuli za hii taasisi na kuipa amri ya kugawa maji kwa haki wakati hizo hatua nyingine zikiendelea kuchukuliwa na Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri, lakini kubwa tunapozungumzia suala la maji, maji ni uhai na maji hayana mbadala na hakuna sababu ya kutoa maji kwa upendeleo. Nimwahidi niko tayari kuongozana na yeye katika kuhakikisha kama ipo changamoto hiyo tuweze kuitatua kwa haraka ili wananchi wa Jimbo la Rombo waweze kupata maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza, pamoja na shukrani nyingi za wananchi wa Bagamoyo kwa Serikali kwa kuwajengea tanki kubwa la maji lita milioni sita Bagamoyo Mjini, naomba kuuliza swali la nyongeza kwamba, sasa ni lini shughuli ya mradi wa kusambaza au kulaza mabomba, mtandao huu mpya wa mabomba ya maji katika Mji wa Bagamoyo na Kata zinazozunguka Mji wa Bagamoyo utaanza kwa sababu tanki lile sasa hivi halileti tija ya kutosha kwa wananchi wa Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua changamoto kubwa sana ya maji katika eneo la Dar es Salaam pamoja na Pwani kwa maana ya Bagamoyo, Serikali imewekeza zaidi ya dola milioni 32 katika kuhakikisha wananchi wa maeneo haya wanapata maji. Nimhakikishie, hii ni hatua ya kwanza na tunamwagiza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Salama Dar es Salaam kuhakikisha mradi huu unaanza haraka ili wananchi wa Bagamoyo waweze kupata maji safi na salama.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada nzuri za Serikali kuwapatia wananchi maji, kuna mradi mmoja wa KfW wa tangu mwaka 2008 ambao ulikuwa uhudumie Mikoa saba ya Manyara, Babati, Mtwara, Kigoma, Lindi na maeneo mengine. Mikoa mingine mitano ilishapatiwa huduma ya maji bado Babati na Mtwara na tulikuwa tumepangiwa shilingi bilioni 20 na kila mkoa shilingi bilioni 10. Mpaka sasa mradi huu haujasainiwa na wenzetu wa Ujerumani pamoja na Serikali ya Tanzania. Naomba nifahamu ni lini mradi huu sasa utasainiwa kwa sababu tunahitaji hizo shilingi bilioni 10 zitusaidie kuondoa tatizo la maji Babati na Mtwara ambako kumesalia.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Babati na mimi nilishafika Babati pamoja na huu mradi mkubwa lakini zipo jitihada pale za utekelezaji wa mradi wa maji. Nataka nimhakikishie, kama tulivyoahidi tutatekeleza lakini tutalifanya hili jambo kwa haraka ili wananchi wake wa Babati waweze kupata maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo Morogoro naishukuru sana Serikali kuona tatizo la Mji Mkuu wa Wilaya ya Hanang na kuweza kuwapangia zaidi ya shilingi bilioni 2. Naomba kuuliza naona kama speed ni ndogo, je, mradi ule utafikisha maji kata 20 kwa sababu wanachotaka kuona wananchi wanakunywa maji na wanatumia maji.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge mama yangu Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu, maeneo yenye changamoto kubwa sana ni katika jimbo lake lakini sisi kama Serikali tuna mradi mkubwa sana pale ambao tumeuwekeza kwa ajili ya kutatua tatizo la maji Hanang. Nataka nimhakikishie sisi kama Wizara na viongozi wa Wizara hii tunamwagiza mkandarasi lazima afanye kazi usiku na mchana, kama atashindwa kufanya kazi ile kwa haraka sisi tutamwondoa tutamweka mkandarasi ambaye anaweza kufanya ile na kuweza kukamilisha mradi kwa mujibu wa mkataba kama ulivyopangwa. Ahsante sana.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, katika majibu yake, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba asilimia 80 ya wananchi wa Kibamba wanapata maji ya bomba, jambo ambalo ni taarifa ya uongo imetolewa Bungeni. Kwa sababu ukiangalia mtandao wa maji ulivyo, kuna maeneo mengi hayana kabisa mabomba ya maji na hata yenye mabomba ya maji, bado kuna maeneo ambayo hayatoi maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoa mfano, kuna kata sita tu Jimbo la Kibamba; Kata ya Goba, Mitaa ya Goba, Matosa, Tegeta A, na kadhalika. Pamoja na Mheshimiwa Waziri kuahidi kwamba Februari maji yatatoka, lakini hayatoki; Kata ya Mbezi, Mitaa ya Mbezi Luisi, Makabe, Msakuzi hakuna kabisa mabomba; Makabe mabomba yapo lakini maji hayatoki; Fijimagohe na Msumi hakuna mambomba; Kata ya Kibamba kule Hondogo, Kibwegere, hakuna mtandao wa maji wa kuwezesha maji kutoka; Kata ya Kwembe, Kinazi B na mitaa mingine kwa ujumla; Kata ya Msigani, maeneo ya Msingwa, maeneo ya Malamba na maeneo mengine yote yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri ametoa jibu la Uongo Bungeni, sasa je, yuko tayari kutoa Takwimu ya ukweli ya hali halisi ya upatikanaji wa maji Jimbo la Kibamba na orodha mtaa kwa mtaa ya upatikanaji wa maji na hatua za utekelezaji? Hilo swali la kwanza.

Swali la pili, siku chache zilizopita, Mheshimiwa Rais akiwa ziarani, amesema kwamba Wizara ya Maji ni kati ya Wizara ambayo ina ma-Engineers wana-perform ovyo ovyo. Kuna miradi mingi ya maji kwa assessment ya Wizara ya Maji ambayo ni miradi hewa, badala ya kutoka maji, inatoka hewa. Sasa kwa kuwa Mheshimiwa Rais ameshatoa hiyo kauli na naamini kauli ya Rais ni agizo:-

Je, Wizara ya Maji iko tayari kuleta Bungeni taarifa ya assessment ya Wizara ya Fedha aliyoisema Mheshimiwa Rais ili tupitie hatua kwa hatua, tuchukue hatua juu ya miradi hewa katika maeneo mbalimbali nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda nimhakikishie kaka yangu Mheshimiwa Mnyika, Serikali imefanya kazi kubwa sana, naye anafahamu kabisa. Kipindi cha nyuma kulikuwa kuna mgao mkubwa sana, lakini sasa hivi kuna utekelezaji zaidi ya asilimia 85 ya upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mnyika anasema taarifa tuliyoisema ni ya uongo. Nisome swali lake kipengele cha (b), anataka kujua ni mitaa ipi katika Jimbo la Kibamba maji hayatoki. Sasa kama Mbunge mitaa yako hujui ipi inayopata maji, unawezaje kuniuliza mimi Mheshimiwa Waziri?

Mheshimiwa Naibu Spika, labda kwa ushauri mdogo tu, nimshauri kaka yangu, afanye ziara katika Jimbo lake, aone kazi kubwa inayofanywa na Serikali. Aende Hodongo aone utekelezaji wa mradi unaofanyika, aende katika katika Kata ya Matosa aone utekelezaji wa miradi unavyofanyika. Nami niko tayari kuongozana naye nikamwonyeshe kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie, anayelala na mgonjwa ndio unayejua mihemo ya mgonjwa. Namshauri aende Jimboni na afanye ziara aone kazi kubwa inayofanyikwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu swali la pili, tunatambua kabisa baadhi ya utekelezaji wa miradi ya maji imekuwa ya kusuasua. Sisi kama Wizara ya Maji tumekuwa tukichukua hatua kwa Wahandisi wababaishaji, lakini pia tumeanzisha Wakala wa Maji Vijijini. Nataka niwahakikishie, tumejipanga vizuri katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Wahandisi wote wababaishaji hawana nafasi katika Wizara ya Maji, tumejipanga katika kuhakikisha Wakalaa huu unaenda kutatua tatizo la maji vijijini. Ahsante sana.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Maeneo ya Mji wa Nachingwea katika Kata za Namatula, Nangwe, Mteruka, pamoja na Kilimanihewa yamekuwa yanapata maji kwa kusuasua sana, lakini wakati huo huo tuna chanzo kikubwa cha maji kinachotokana na chanzo cha maji ya Mbwinji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua mpango wa Serikali juu ya kutoa fedha ili kuweza kufanya utanuzi wa kusambaza maji katika maeneo ambayo nimeyataja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nampongeza Mheshimiwa Mbunge. Nimepata nafasi ya kutembelea katika Jimbo lake, lakini kiukweli katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji, lazima tuangalie namna gani tunaweza tukatumia kile chanzo kikubwa cha Mbwinji. Sisi kama Wizara ya Maji tuko tayari na tumejipanga katika kuhakikisha tunatafuta fedha ili tuweze kutumia chanzo kile cha maji ili wananchi wake waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Tatizo la maji la Jiji la Dar es Salaam linafanana kabisa na tatizo la maji la Jiji la Mbeya. Katika Jiji la Mbeya, wataalam wameshasema, solution ya tatizo ni kutoa maji kutoka mto Kiwira, feasibility study imeshafanyika, taarifa tunazo na mto Kiwira hauko mbali, ni kilomita chache sana kutoka Mbeya. Naamini Mheshimiwa Waziri anajua hata bajeti inayotakiwa kutokana na ile feasibility study.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini fedha itapelekwa katika ile project ili ile project ifanyike tuondoe tatizo la maji kwenye maeneo ya Uyole, Mwakibete na hususan maeneo kama Shewa ambako wananchi wanapata taabu sana na wako Jijini, wanalipa kodi za Jiji.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge wa Jiji la Mbeya, kaka yangu Sugu, amezungumza suala la msingi sana. Kweli tunatambua kabisa katika suala zima la maji katika Jiji la Mbeya kumekuwa na ongezeko kubwa sana la watu, lakini tunaona kabisa tukiyatoa maji mto Kiwira na kuyaleta tutakuwa tumetatua kabisa tatizo la maji. Nataka nimhakikishie kwamba utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga katika kuhakikisha kupitia mapato yetu ya ndani lakini pia kwa wafadhili mbalimbali tupate fedha ili tuwekeze na wananchi wa Mbeya waondokane na tatizo hili la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na Wizara ya Maji kuhakikisha inawafikishia wananchi wote maji Tanzania, lakini kumekuwa na kero kubwa na mbaya zaidi kutoka Wizara ya Maji ya kubambikia wananchi bili.

Je, ni lini Wizara hii itaweka mkakati wa kutatua kero hii kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni haki ya mwananchi kupatiwa maji, lakini pamoja na haki hiyo ya kupatiwa maji, mwanachi naye ana wajibu wa kulipia bili za maji, lakini siyo kulipia tu, anatakiwa alipie bili za maji ambazo siyo bambikizi. Sisi kama viongozi wa Wizara tumeshawaita Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Maji na tukawapa agizo na kuwaandikia hadi mkataba, kwa maana ya kuhakikisha kwamba hili tatizo wanaliondoa kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba ambao tumekubaliana ni katika kuhakikisha Mamlaka zote tunatoka sasa katika mfumo wa zamani tuwe katika pre-paid meter. Nataka nitumie nafasi hii tena kuwaagiza kuanzisha suala zima la pre-paid meter katika kuhakikisha tunaondokana na malalamiko haya ili kuhakikisha kwamba wananchi wanalipia maji kadri wanavyotumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa asilimia ya upatikanaji wa maji katika Mji wa Tunduru pamoja na vijiji vyake 92 ni wa chini sana; na kwa kuwa Serikali imekuwa ikitoa fedha kidogo kidogo katika mradi mkubwa wa Tunduru:-

Je, Serikali haioni sababu sasa ya kutafuta fedha za kutosha ili mradi huu ukamilike kwa haraka na wananchi waweze kupata maji kwa urahisi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, vijiji vya Lakalola, Nakachindu, Namwanga, Nangwale, Tupendane, vimekuwa vikikabiliwa na tatizo kubwa sana la maji katika Jimbo la Lulindi pamoja na kule Rivangu na Wakandarasi wako site; kuna OBD and Company na Sing Lyimo Enterprises, lakini tangu wapeleke certificate mwezi Novemba, 2018 hadi sasa Wakandarasi hao hawajapata fedha zao ili kuendelea na kazi:-

Je, nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Niwe mkweli, tuna changamoto kubwa sana Tunduru na hata Mkoa wa Ruvuma, tulifanya ziara tukaona changamoto hiyo. Kubwa tunaloliona, tuna ubabaishaji mkubwa sana wa Mhandisi wetu wa Maji wa Mkoa. Sisi kama Wizara tumeshamwondoa na tutaendelea kuwaondoa Wahandisi wote wababaishaji katika Wizara yetu ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa tunatambua kabisa utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha. Tulikuwa tuna madai zaidi ya shilingi bilioni 88 ya Wakandarasi. Tunashukuru sana Wizara ya Fedha imetupa shlingi bilioni 44, tumeshaanza kuwalipa Wakandarasi na mwezi huu wa Nne mwishoni watatupa shilingi bilioni 44 nyingine katika kuhakikisha tunawakamilishia Wakandarasi madai wanayotudai. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha miradi ya maji inakuwa endelevu na kuweza kuwahudumia wananchi. Ahsante sana.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri na ninashukuru pia kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na Waziri wake na Katibu Mkuu wake. Ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba alituma wataalam kule Kata ya Kanigo, Kata ya Kashenye, Kata ya Ishozi na Kata ya Ishunju kwa ajili ya maandalizi ya awali ya kutumia maji ya Ziwa Victoria. Je, yuko tayari kuharakisha jitihada hizo ili maji hayo yaanze kutumika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali dogo la pili. Kwa kuwa Wilaya ya Misenyi tumebarikiwa kuwa na mito mingi; tunao Mto Kagera pamoja na Mto Nkenge na mingine: Je, mradi kama huu ambao uko mbioni kuanza kama Mheshimiwa alivyojibu katika maeneo ya Kyaka na Bunazi, atakuwa tayari kubuni mradi kama huo katika maeneo yaliyo karibu na Mto Nkenge?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya. Nilifika katika Jimbo lake, nimeona kazi kubwa zinazofanyika katika eneo lile. Kubwa ambalo ninalotaka nimhakikishie, sisi kama Wizara ya Maji ambayo siyo Wizara ya ukame, tumeona haja kwamba haina budi na kwamba haiwezekani tuone kabisa vijiji ama Miji ambayo iko karibu na mito mikubwa ama maziwa wakose maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tuna vyanzo vya uhakika, ndiyo maana tumewatuma wataalam wetu waweze kwenda katika eneo lile ili tuweze kubuni mradi na wananchi wake waweze kupata majisafi na salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la ku- design katika Mto Nkenge; uwepo wa chanzo unatupa nafasi kama Wizara ya Maji katika kuhakikisha tunabuni miradi mikubwa ili tuweze kuwapatia wananchi wake maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kuanzisha mradi katika Mto Nkenge ili wananchi wake waweze kupata majisafi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa upo mradi wa maji ambao tunautegemea sana katika Wilaya ya Ngara, mradi ambao tayari umeshapata kibali cha Serikali; na mwaka huu unaoishia kwenye bajeti zilikuwa zimetengwa shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuanza usanifu wa mradi huu.

Ni lini Mhandisi Mshauri atakuwepo site tayari kwa ajili ya kuanza usanifu wa mradi huu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, binafsi nilipata nafasi ya katika Jimbo lake la Ngara na tumeona chanzo cha Mto Ruvubu ni chanzo cha uhakika na kina maji mengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama viongozi wa Wizara ndiyo maana tukamtuma mtaalam wetu. Kwa hiyo, kubwa tutafanya kila linalowezekana kuhakikisha Mhandisi Mshauri anapatikana kwa haraka ili kazi iweze kuanza mara moja na wananchi wake waweze kupata mradi huo.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa majibu yanayotia matumaini kama yatatekelezeka, kwa sababu mradi wa Ziwa Victoria kuanzia wakati wa Mheshimiwa Eng. Kamwelwe alisema mnafanya upembuzi yakinifu na mradi ungeenda kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mji wa Tarime ndiyo Makao Makuu ya Wilaya Tarime na umekuwa na matatizo ya maji kwa muda mrefu na kusababisha wananchi wasifanye shughuli zao za maendeleo; na kwa kuwa vyanzo vikuu katika Mji wa Tarime ni Bwawa la Nyanduruma na lile la Tagota ambalo halitoi majisafi na salama na Wizara tuliowaomba hata angalau wajenge treatment plant wakasema wanategema mradi mkubwa wa Ziwa Victoria:

Ni lini sasa mtahakikisha kwamba ule mradi ambao tumeuanzisha Gamasara ambao tumesha-rise certificate, Mkandarasi amesimama kuanzia Novemba tumeleta Wizarani mpaka leo hajalipwa, ni lini yule Mkandarasi atalipwa ili angalau ajenge lile tenki la lita 100,000 kuweza kusaidia wananchi wa Gamasara na Kata ya Nyandoto na Kata za pembezoni kwa kipindi hiki tukisubiria huu mradi wa Ziwa Victoria ambao mmesema unakwenda kuanza mwaka 2019/2020?

La pili, hawa DDCA wameshakamilisha na walileta certificate na hata Mheshimiwa Eng. Kamwelwe mimi mwenyewe nilimpa document, lakini mpaka leo inavyosemekana, hawajalipwa fedha na ndiyo maana hata hawajaanza kufanya huo utafiti wa maji ya chini ya ardhi kama mlivyo-report hapa. Napenda sasa nihakikishiwe leo kwamba hawa DDCA watalipwa fedha ili wananchi wa Tarime hasa zile Kata za pembezoni waweze kuchimba visima na wapate majisafi na salama. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimtoe hofu dada yangu Mheshimiwa Esther Matiko, Serikali ya Awamu ya Tano ikiahidi inatekeleza na ikichelewa kutekeleza, basi kunakuwa na sababu maalum ya kueleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ninalotaka kusema, pamoja na mradi mkubwa huo wa Ziwa Victoria katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji Tarime, lakini tuna mradi pale Gamasara wa asilimia 25, lakini tunatambua kabisa utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri, tulikuwa na madeni ya Wakandarasi zaidi ya shilingi bilioni 88, lakini tunamshukuru Mheshimiwa Rais amewaagiza watu Wizara ya Fedha kutupa zaidi ya shilingi bilioni 44 kwa ajili ya kuwalipa Wakandarasi na tumeshazipata na tumeshazigawa. Tuna shilingi bilioni 44 nyingine tutakazopewa mwezi huu wa Nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie, katika maeneo yote ambayo Wakandarasi wanadai, tutawalipa ili miradi iendelee kutekelezeka na ahadi ya kumtua mwana mama ndoo kichwani iweze kitimilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la DDCA, sisi pale tumeona haja ya uchimbaji wa visima. Sasa katika mgao huo wa shilingi bilioni 44, watu ambao wamelipwa ni watu wa DDCA. Tunawaagiza waende Tarime haraka katika kuhakikisha hii kazi inafanyika ili ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mwana mama ndoo kichwani inatimilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba endeleeni kutuunga mkono bajeti yetu katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. JOHN. W. HECHE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Swali hili limekuja wakati mzuri kwa sababu ni swali linalohusu Tarime na ilikuwa Wilaya moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Rais amekuja Tarime Mwezi Julai, alisimama kwenye Mji wa Nyamongo kwenye Kijiji cha Kewanja na akaahidi kwamba Mwezi wa Tatu mwaka huu, watu wa Nyamongo ambao ni zaidi ya 35,000 wakazi wa pale na wakazi wa Sirari watakuwa wamepata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Naibu Waziri anasemaje kuhusu hilo likiendana sana hasa na swali hili ambalo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Mwezi Julai?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimjibu tu kwa ufupi Mheshimiwa Mbunge. Ahadi ni deni; na Mheshimiwa Rais anapoahidi sisi hatuna kikwazo cha kushindwa kutekeleza. Kwa hiyo, tumejipanga katika kuhakikisha tunalitekeleza hilo jambo ili wananchi waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wabunge tunachimba visima kwenye maeneo yetu. Kisima cha mita 100 kina-cost takribani shilingi milioni saba, lakini ukienda Halmashauri kisima cha mita 100, gharama zinazolipwa ni zaidi ya shilingi milioni 35 kwa kisima kimoja. Visima hivi 23 ambavyo vinataka kuchimbwa Tarime vitagharimu siyo chini ya shilingi milioni 900 kwa bei za Wakandarasi na bei za hao wanaokwenda huko kwenye Halmashauri zao.

Je, Serikali sasa lini ita-revisit bei hizi na kutoa bei elekezi kuhakikisha pesa za Serikali zinaokolewa na ubadhirifu ili wananchi wapate maji kwa bei nafuu ambapo yanaweza kupatikana kwa shilingi milioni saba tu kwa kisima cha mita 100?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nampongeza sana Mheshimiwa Zungu kwa swali lake zuri sana lakini kubwa tukiri kwamba kulikuwa kuna ubadhirifu mkubwa sana hasa katika miradi ya maji. Sisi tumeona hilo na ndiyo maana tukaanzisha Wakala wa Maji Vijijini na tuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kutupitishai Muswada wetu na sisi tumejipanga katika kuhakikisha tunasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya msingi katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na gharama nafuu, sisi tunataka tuuongezee uwezo kwa Wakala wa Maji wa Uchimbaji Visima (DDCA) katika kuhakikisha tunawapa vifaa vya kutosha ili uchimbaji wake uwe nafuu uweze kuendana na watu binafsi. Ahsante sana.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwanza naipongeza Serikali kwa hatua ambayo imechukua kuweza kuhakikisha kwamba kuna mradi wa maji wa kutoka Ziwa Victoria, Katoro, Buseresere. Wananchi wanahitaji kujua ni lini utekelezaji utaanza rasmi?

Swali la pili; kwa kuwa azma ya Serikali mpaka mwaka 2020 ni kuhakikisha kwamba mijini asilimia 95 ya maji, asilimia 85 vijijini, jambo ambalo nikiangalia hali halisi, kwa mfano katika Mkoa wa Geita Jimbo la Busanda, naona hali iko chini sana. Napenda kujua sasa kwamba nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba tunapata maji kwa asilimia 85 katika Jimbo Busanda na asilimia 95 Mji wa Geita ambapo sisi wananchi wote ni Makao Makuu ya Mkoa wetu wa Geita?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nampongeza sana Mheshimiwa Lolesia kwa kazi nzuri sana ya kuwapigia wananchi wake. Kubwa, tunatambua kabisa maji hayana mbadala. Ndiyo maana sisi kama Wizara ya Maji tumefanya jitihada ya kuwasilisha hili andiko kwa Wizara ya Fedha ili waweze kuwasilisha EIB. Wizara ya Maji itafanya ufatiliaji wa karibu katika kuhakikisha jambo hili linakamilika kwa wananchi wake ili mradi uweze kuanza kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha azma ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mwanamama ndoo kichwani na kutimiza Ilani ya Chama cha Mapinduzi asilimia 85 ya upatikanaji wa maji vijijini na asilimia 95 ya upatikanaji mijini, tumeshakamilisha miradi zaidi ya mitatu katika Jimbo lake. Moja, Nyakagongo, Luhuha pamoja na Mharamba katika kuhakikisha wananchi wale wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati uliokuwepo sasa hivi ni katika kuhakikisha tunakamilisha mradi wa zaidi ya shilingi bilioni nne wa Nachankorongo ili mradi ule ukamilike kwa wakati na umeshafikia zaidi ya asilimia 90 upo katika muda tu wa matazamio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa na la msingi kabisa, sasa hivi tunakamilisha mradi wa Lamugasa na tunajenga mradi wa maji Nkome, Nzela ambao ni wa zaidi ya shilingi bilioni 25 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji katika miji 25 katika mpango wa kutatua tatizo la maji, Mkoa wa Geita tumeuangalia kwa ukaribu zaidi na tunafanya jitihada kubwa ya kutatua tatizo la maji.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Kwa kuwa Bwawa la Yongoma, katika Mto wa Yongoma lilikuwa-designed na Serikali ya Japan kupitia JICA tangu 2012; na kwa kuwa mwaka huu 2018/2019 liliwekwa kwenye bajeti kwamba lijengwe, Serikali inatoa tamko gani kuhusu ujenzi wa bwawa hili?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Kaboyoka. Kubwa ambalo nataka niseme ni utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Nia ya Serikali bado ipo pale pale, na sisi kama Wizara tunaendelea kuhakikisha fedha hizi zinapatikana ili bwawa lile liweze kujengwa na wananchi waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mji wa Liwale ni Mji unaokua kwa haraka sana na una chanzo kimoja tu cha maji; na kutokana na mabadiliko ya tabianchi, chanzo kile hakitoshelezi tena. Je, ule mradi wa kutafuta chanzo mbadala cha maji kwa Mji wa Liwale, umefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, lakini na pili nimepata nafasi ya kufika katika Jimbo lake la Liwale. Pamoja na jitihada kubwa za Serikali zinazofanyika lakini kiukweli, Liwale kuna changamoto. Sasa sisi kama Wizara tulishawaagiza watu wetu wa rasilimali za maji katika kuhakikisha wanafanya utafiti wa kina ili tuweze kupata chanzo cha uhakika, tuweze kubuni mradi mkubwa ambao kwa ajili ya kutatua kabisa tatizo la maji Liwale. Nataka nimhakikishie sisi tutalifanya jambo hili kwa haraka ili wananchi wake wa Liwale waweze kupata maji ya uhakika.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Miradi ya maji katika Vijiji vya Matala, Kansay, Buger, Endonyawet na Getamock Wilayani Karatu chini ya mpango wa WSDP imejengwa chini ya kiwango na hivyo haifanyi kazi, karibu shilingi bilioni nne zimetumika na haziwanufaishi wananchi. Tulimwomba Mheshimiwa Waziri mara nyingi aje Karatu ili aje atatue tatizo hilo…

MWENYEKITI: Uliza swali sasa.

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba awaambie wananchi wa vijiji hivyo ni lini atakwenda ili kutatua changamoto za miradi hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge, binafsi nilishapata taarifa za Karatu na nimefika, lakini kubwa kuna miradi ambayo imefanyiwa ubadhirifu. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Viongozi wa Wizara tumesha-note na tumekubaliana tutakwenda katika maeneo yale yote na wale walioshiriki katika ubadhirifu ule, lazima fedha watazitapika na hatua kubwa kali tutazichukua.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Mradi wa bomba la Ziwa Victoria umeshafika katika Halmashauri ya Mji wa Kahama, lakini usambazaji katika Kata nyingi bado haujafanyika, Kata ya Mwenda kulima, Kagongwa, Iyenze, Isagee maji hayajafika. Je, Serikali ina mpango gani wa kusambaza maji ya Ziwa Victoria ili wananchi waweze kunufaika? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza tutambue jitahada kubwa zilizofanywa na Serikali, tunatambua kabisa tulikuwa na changamoto kubwa sana, katika Mji wa Kahama na Shinyanga na Serikali ikaona haja sasa ya kuyatoa maji Ziwa Victoria kwa ajili ya kutatua matatizo haya ya maji, kikubwa maji yale yamekwishafika lakini imebaki changamoto tu ya usambazaji. Hivyo, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge, wali wa kushiba unaonekana kwenye sahani, sisi tumekwishawaita Wakurugenzi wote na tumekwishawaagiza katika mapato yao wanayoyakusanya watenge asilimia katika kuhakikisha wanasambaza maji kwa wananchi ili waweze kupata maji safi salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba anijibu swali langu la nyongeza. Mheshimiwa Waziri alifika katika Kata ya Ruaha Mbuyuni na akaona jinsi matatizo ya maji yanavyosumbua. Wananchi wamekuwa wakipata kipindupindu kila mwaka na yeye aliahidi mambo makubwa. Sasa je, ni lini wananchi wa Ruaha Mbuyuni ambao wanategemea kupata kituo cha afya watapata maji pale?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze Mbunge wa Kilolo, Mzee wangu, kwa kazi kubwa sana anayoifanya, lakini tulipata nafasi ya kufika Ruaha Mbuyuni. Changamoto kubwa tuliyoiona kwa Wahandisi wetu walitengeneza tenki la maji lakini hawakuwa na chanzo cha maji. Kwa hiyo tuliwaagiza watu wa rasilimali za maji wa bonde lile waende na wameshafanya tafiti kikubwa tunawaagiza watu wa DDCA waende kuchimba kisima haraka katika kuhakikisha mradi ule unafanya kazi kwa wakati.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa ongezeko la watu na hasa Jiji la Dodoma limekuwa kubwa baada ya Makao Makuu kuhamia Dodoma, je, Serikali ina mpango kabambe au mkakati gani wa kuhakikisha kwamba maji ya Ziwa Victoria yaliyofika Tabora yanafika Dodoma kuwasaidia wananchi wa Dodoma kutokana na upungufu wa maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Bura kwa swali lake zuri sana, sisi kama Wizara ya Maji tunatambua kabisa sasa hivi kumekuwa na ongezeko kubwa sana katika Mkoa huu wa Dodoma, lakini jitihada kubwa ambazo tulizozifanya sasa hivi, uzalishaji wetu zaidi ya lita milioni 55, lakini mahitaji lita kama milioni 44. Kwa hiyo, tuna maji kwa kiasi kikubwa, kubwa ambalo tunaloliona hapa ni suala zima la usambazaji, lakini itakapobidi tutafanya kila jitihada katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji na wananchi wa Dodoma wasipate tatizo hilo.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kutokana na shida kubwa ya maji hapa nchini, Bunge hili lilitengeneza, liliunda Wakala wa Maji, sasa ningependa kujua, je, tayari, Serikali imeshatengeneza kanuni za huo Wakala na kama zitagawiwa kwa Wabunge?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nilipongeze sana Bunge lako Tukufu kutokana na jitihada kubwa walizofanya kupitisha Muswada wetu, pia kwa namna ya kipekee tumshukuru sana Mheshimiwa Rais. Baada ya Bunge kupitisha Muswada ule, Mheshimiwa Rais ameshasaini na imeshakuwa Sheria, sisi kama Wizara ya Maji, tutazileta kwa haraka kanuni zile ili tuanze utekelezaji kwa haraka sana. Ahsante sana.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda nimuulize Waziri, kwa kuwa kuna mradi mkubwa wa maji kutoka Nyamtukuza katika Wilaya ya Nyang’hwale, kupita Kakora, Kitongo, Ikangala, Kharumwa, Izunya hadi Bukwimba ambao umekuwa ukisuasua kwa muda mrefu, lakini Serikali ikiwa ikitoa pesa. Je, ni lini sasa mradi huu utakamilika na namwomba Mheshimiwa Waziri baada ya Bunge hili aende akauone mradi huo kwa nini unaendelea kusuasua?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge. Kubwa pamoja na mradi huo, lakini tumeshalipa zaidi ya bilioni moja na milioni mia saba certificate yake kwa Mkandarasi anayedai, ili mradi usikwame.

Kuhusu kusuasua kwa mradi, sisi kama Wizara ya Maji, Wahandisi ama Wakandarasi wababaishaji tutawaweka pembeni, nataka nimhakikishie kabla ya Bunge tutakwenda Nyang’hwale katika kuhakikisha tunaenda kuukagua mradi ule na ikibidi kama Mkandarasi hana uwezo wa kutekeleza mradi huo tutamwondoa mara moja. Ahsante sana.
MHE. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu swali vizuri na naishukuru Serikali kwa jitihada zake zinazoelekezwa Hangang’ hasa ziwe Bassotu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, ni kweli visima vimechimbwa, lakini nafikiri ni Wilaya ya peke yake ambayo zimewekwa solar ambazo hazina betri na ni Wilaya ambayo temperature yake iko chini kwa hiyo maji hayapatikani kila wakati. Sasa nataka kujua wakati kwingine kunawekwa solar za betri kwa nini Wilaya ya Hanang’ katika visima mbalimbali vilivyochimbwa kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri hawakuweka betri hizo na hasa Masakta ambapo ilipangiwa shilingi bilioni 1.2 mpaka leo tatizo liko palepale?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Wilaya ya Hanang’ iko kwenye bonde la ufa na kwa hivyo kuna joto chini, kwa hiyo kupata maji kwenye visima ni ngumu sana. Sasa nataka Mheshimiwa Naibu Waziri anieleze kama bwawa linalotakiwa Dirma linachimbwa na bwawa la Gehandu na Gidahababieg linachimbwa kusudi tatizo hilo la ujumla la Hanang’ liweze kukabiliwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana mama yangu Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu kwa kazi kubwa anayofanya. Ni miongoni mwa wamama ambao wamejitoa kupigania suala zima la maji katika jimbo lake la Hanang.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la kwanza la changamoto ya betri, nimuagize Mhandisi wa Maji wa Mkoa wa Manyara afuatilie kwa haraka ili changamoto hizi tuweze kuzitatua kwa haraka ili wananchi wake waendelee kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yenye ukame au yaliyopitiwa na bonde la ufa, uchimbaji wa visima imekuwa ni changamoto kubwa sana, mfano Dilma. Sisi kama Wizara ya Maji tumeona haja sasa ya kuchimba mabwawa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika uchimbaji wa mabwawa ili wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu na kuweza kumtua mwanamama ndoo kichwani. Ahsante sana.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Hali ya upatikanaji wa maji katika kijiji hicho ni mbaya sana, ukiongea habari ya vituo vitatu kwa wananchi zaidi 5,000 ni chini kabisa ya kiwango ambacho kinaruhusiwa. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Mheshimiwa Waziri anajua Halmashauri ya Wilaya ya Karatu ina idadi ndogo ya watumishi katika sekta ya maji na kazi za kitaalam alizozielekeza kwa idadi ya wataalam tulionao haitaweza kukamilika. Je, yuko tayari sasa kuongeza nguvu ya uhandisi na wataalam wa survey ili kazi hiyo aliyoelekeza ifanyike kwa muda unaotakiwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, vyombo vya watumia maji, mfano, Bodi za Maji, Mamlaka Jumuiya za Watumia Maji na Kamati za Maji zinatambulika kisheria na vimetoa huduma za usimamizi na uendelezaji wa miradi ya maji. Hivi karibuni Serikali imesimamisha uchaguzi wa chombo cha maji kinachoitwa KAVIWASU pale Karatu ambacho kimetoa huduma hiyo kwa zaidi ya miaka 20. Je, ni halali Serikali kuingilia mchakato wa kupata viongozi wa wananchi ili waweze kusimamia chombo chao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri, lakini kubwa sisi kama Wizara ya Maji tunatambua changamoto kubwa sana ya maji Karatu na ndio maana tuna mradi mkubwa sana wa TOM zaidi ya milioni 650 ambao tunautekeleza. Kikubwa tunatambua utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na watumishi wa kutosha wenye weledi na wenye uwezo na sisi kama Wizara ya Maji ndio maana tukaja na Wakala wa Maji. Nataka nimhakikishie uanzishwaji wa wakala ule tutahakikisha tunaweka wataalam wetu wa kutosha na katika eneo lake ili mwisho wa siku wananchi wa Karatu waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu chombo cha watumiaji maji, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hilo nimelipokea hebu tulifuatilie kwa ukaribu ili tuweze kulitolea ufafanuzi wa haraka. Ahsante sana.
MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimesikiliza majibu ya Naibu Waziri na kwa kuwa Serikali imepokea andiko hilo, naamini kwamba italichukulia kwa uzito ili kunusuru wananchi hususan akina mama katika Kata za Mlimba na kata za jirani na Jimbo la Mlimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, mkandarasi aliyemaliza Mradi wa Maji Msolwa - Kilombero ambaye hajalipwa fedha zake na Serikali lakini amekubali kuendelea kufanya ujenzi katika Mradi wa Mbingu. Je, Serikali ipo tayari kumlipa fedha zake za awali alizozilimbikiza na anaidai Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kulikuwepo na mpango wa kuongeza kina katika bwawa la Mindu Manispaa ya Morogoro kutokana na maji yaliyopo kutotosheleza wananchi wa Manispaa ya Morogoro. Kwa miaka mitatu sasa Serikali imesambaza mabomba katika Kata za Kiega A na B, Kihonda, Mkundi, je, ni lini itapeleka maji kwa wananchi hao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Mimi nilipata nafasi ya kufika katika jimbo lake lakini kubwa ambalo tumeona tuna changamoto kubwa pale Mlimba lakini tumefanya jitihada ya uchimbaji wa visima lakini bado kumekuwa na changamoto. Tumeona haja sasa ya kutafuta chanzo cha kutosheleza kuhakikisha wananchi wa Mlimba wanapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu fedha anazodai mkandarasi anayetekeleza mradi wa maji, tunashukuru sana Wizara ya Fedha ilitupatia kiasi cha shilingi bilioni 44 kwa ajili ya malipo ya wakandarasi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo kumlipa fedha zake kwa wakati ili aendelee kutekeleza mradi na wananchi waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la maji Manispaa ya Morogoro, kiukweli Morogoro Mjini kuna changamoto ya maji na hii yote imetokana na sababu tu ya ongezeko la watu na hata shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Sisi kama Wizara ya Maji tumefanya jitihada kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha kufanya mazungumzo na Serikali ya Ufaransa kwa ajili ya uwekezaji wa fedha kwa maana ya utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha. Zaidi ya Euro milioni 70 zitakazopatikana zitawekezwa katika Mji ule wa Morogoro ili kuhakikisha tunaongeza kina cha Bwawa la Mindu ili wananchi wa Morogoro waweze kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza. Sisi kama Wizara ya Maji tutafanya jitihada za haraka ili jambo hili liweze kutekelezeka na wananchi wa Morogoro waweze kunufaika na huduma hii muhimu. Ahsante sana.
MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Mradi wa Maji Handeni pamoja Korogwe yaani Handeni Trank Main ambao tuliahidiwa kuwemo katika miradi ya miji 28 ambayo inategemea fedha kutoka Serikali ya India na naamini kwamba fedha hizo tayari zimepatikana. Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza mradi huu ili wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, dada yangu Mboni amekuwa mpiganaji mkubwa sana hususani katika suala zima la maji katika Jimbo lake la Handeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tulipata nafasi ya kutembelea katika jimbo lake na tumeona kabisa hii changamoto. Ndiyo maana Wizara yetu ya Maji tukaona katika miji hiyo 28 ambayo inatakiwa ipatiwe maji haraka ni mmojawapo ni Jimbo lake la Handeni. Nataka nimhakikishie sasa hivi tupo katika hatua ya kumpata Mhandishi Mshauri na mkadarasi ndani ya mwezi Septemba atakuwa amekwishapatikana na miradi hii itatekelezwa katika maeneo yote ili kuhakikisha tunamtua mwanamama ndoo kichwani.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyikiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri amefika Jimbo la Mbuli Vijijini na ameona changamoto iliyopo hapo inayofanana na Jimbo la Mlimba. Mheshimiwa Naibu Waziri aliahidi kisima kichimbwe Hyadom na tumeomba shilingi milioni 80 na akaahidi itatumwa. Je, ni lini sasa atatupatia fedha za kuchimba kisima pale Hyadom?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri sana anayofanya katika jimbo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilifika pale Hyadom tumeona kuna mradi mkubwa lakini katika kuhakikisha tunawaongezea chanzo kwa maana ya uzalishaji tukaona kuna haja ya uchimbaji wa kisima. Sisi tuna Wakala wa Uchimbaji Visima (DDCA), kwa hiyo, niwaagize wachimbe kisima kile haraka ili wananchi wa Hyadom waweze kupata ongezeko la maji na waweze kupata huduma hii muhimu.
MHE. GIMBI D. MASABA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja namajibu ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Mradi wa Ziwa Victoria, ulikuwa na mabomba mawili makubwa, bomba la kwanza ni bomba la maji safi na salama nabomba la pili ni bomba la maji ambayo hayana dawa kwa matumizi ya mifugo na mengineyo. Sasa naomba kufahamu kama mkataba huu umezingatia ufanisi wa mradi huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tumekuwana miradi mingi ambayo tunayo katika bajeti ambayo sasa hivi inakamilika hususan Mradi wa Nyangokulwa, Mradi wa Nyakabindi, Mradi wa Sanungu na Mradi wa Mahina. Miradi hii bado haijatekelezeka na kwenye kitabu cha Waziri nimeona kama miradi 10 ambayo wametupa. Sasa nataka kufahamu, ni kwa nini Serikali inatupa miradi ambayo haitekelezeki?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote wa Simiyu akiwemo Mtemi Chenge pamoja na Mheshimiwa Mbunge Mpina, kwamba leo ni siku muhimu sana kwa Wanasimiyu kwamba ule mradi ambao umeahidiwa na Serikali kwa muda mrefu sana ninavyozungumza Katibu Mkuu yuko Dar es Salaam anasaini financial agreementkwa ajili ya utekelezaji wa mradi mkubwa huu wa maji Simiyu.

Kwa hiyo, kikubwa hii ni Serikali ya awamu ya tano inapoahidi inatekeleza. Hata hivyo, kikubwa cha msingi kuhusu suala zima la utekelezaji wa mkataba, nataka nimakikishie, design au mkataba jinsi ulivyotuelekeza na sisi ndivyo tutakavyotekeleza mradi ule kama tulivyoelekezwa na mkataba.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, kuhusu miradi ambayo tumeahidi kwa ajili ya utekelezaji, sisi kama Wizara ya Maji zipo changamoto, moja, kulikuwa na miradi ambayo ilikuwa inahitaji kulipwa certificate, tumeshapokea bilioni 44 zingine na moja ya watu ambao tumewalipa ni wakiwemo Wanasimiyu, lakini kikubwa tumewatengea tena katika bajeti hii bilioni tano na milioni 950, yote katika kuhakikisha tunatatua matatizo ya maji.

Mheshimiwa Spika, nataka nimwagize Mhandisi wa Maji wa Mkoa wa Simiyu, ahakikishe fedha hizi zinatumika katika kuhakikisha wanakamilisha miradi ya maji na wananchi wa Simiyu waweze kupate maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.

SPIKA: Kabla hujaoondoka Naibu Waziri, kabla hujaondoka hapo, kidogo tu, rudi hapo. Kuna ufafanuzi wa Itilima, itaguswa na Kisesa kwa Mheshimiwa Mpina.

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, bila shaka.
MHE. HAWA MCHAFU CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushuru pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri sasa ningependa nimuulize maswali wadogo wawili yangongeza. Tunaishukuru sana Serikali kwa kuikabidhi miradi ya serikali kwa DAWASA ikiwemo mradi wa Bokomnemela Vikuruti na Ngeta.

(i) Ni lini sasa DAWASA itakamilisha zoezi la ufangaji maji majumbani ikizingatiwa wananchi wanauhitaji mkubwa wa maji na hivi tunavyozungumza ni nyumba 30 tu zilizofungwa kati ya wananchi wote walojaza fomu?

(ii) Nataka kujua ni kwanini DAWASA wanafanya ucheleweshaji wa kijiji cha kipangege Kata Soga. Kijiji hakipati maji ya kuridhisha presha yake ni ndogo na wakati mwingine hakuna kabisa maji nataka kusikia kauli ya Serikali inasema nini juu ya uchelewashi huu unaofanywa na DAWASA?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma ni miongoni mwa Wabunge makini katika ufuatiliaji na kupigania maendeleo ya watu wake katika Mkoa wa Pwani. Lakini kikubwa maji hanaya mbadala sasa niagize Mkurugenzi wa Mamlaka wa Majisafi na Usafi wa Mazingira DAWASA Eng. Luhemeja katika kuhakikisha suala la ufungaji mita kwa wananchi lakini pia mradi huu wa Soga uwezi kukamilika kwa wakati ahsante sana.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na niweze kuuliza wali la nyongeza. Kwa kuwa matatizo yanayowapata watu Kibaha yanafanana na watu wa kigamboni

Je Serikali ina mpango gani wa kukamilisha mradi wa visima vya Kimbiji na Mpera ili wananchi wa Kigamboni, Tuangoma, Chamazi na Mbagala waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya lakini kikubwa katika kuhakisha tunatatua tatizo la maji katika Mkoa wa Dar es Salaam. Wizara yetu ya maji kupitia Wizara ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira DAWASA imechimba visima zaidi ya 20 Mpera na Kimbiji. Sasa agizo la Mheshimiwa Waziri nikuhakisha visima vitano wanatangaza tenda mkandarasi ampatikane ili wananchi wa maeneo ya Kigamboni na Mbagala waweze kupata maji safi, salama na ya kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tupo katika hatua hiyo tunataka mkandarasi akapopatikana kazi ianze mara moja na wananchi hawa waweze kupata maji.
MHE. PETER A. P. LIJUALIKALI: Mheshimiwa Spika, nafahamu Serikali imetoa msamaha wa kodi kwenye miradi yake lakini natamani nifahamu ni kwa nini sasa miradi ya watu binafsi wanaofanya kazi hii wenyewe hawapati misamaha? Maana yangu ni kwa nini kwenye vifaa vingine watu wanaofanya kazi hizi hawapati misamaha ya kodi ili kusaidia Serikali kupeleka huduma hii? Msamaha huu ungekuwa inclusive yaani usiwe tu kwa watu wanaofanya kazi Serikali peke yake. Kwa hiyo, napenda kufahamu ni kwa nini watu wengine pia hawapati misamaha huo?

Mheshimiwa Spika, pia naomba nifahamu kama Mheshimiwa Waziri atakubali kwenda nami sambamba kwenye Jimbo langu hasa kwenye Kata za Kipangalala na Kibaoni ambako kuna miradi mikubwa ya maji ya takribani shilingi milioni 600 lakini ni kama vile imesimama na fedha hizi ni kama zimelala. Kwa hiyo, naomba nifahamu commitment ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwa sababu anafahamu haya mambo nilishakaa naye ofisini kwake na kuzungumza kwa kirefu.

Kwa hiyo, naomba nijue kama yuko tayari twende Jimboni kwangu ili tukaone nini shida na tupate majibu kwenye mambo haya. Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri lakini kubwa sisi kama Wizara ya Maji lengo letu na nia ya Mheshimiwa Rais ni kumtua mwana mama ndoo kichwani na kuhakikisha Watanzania waishio mijini na vijijini wanapata maji safi salama na yenye kuwatosheleza. Kwa mazingatio na ushauri wako niseme tu kwamba tumepokea ushauri na tutaufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la commitment ya mimi kuongozana naye katika Jimbo lake, Mheshimiwa Lijualikali mimi sina kikwazo chochote, nipo tayari kuhakikisha tunakagua miradi ya maji. Ahsante sana.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka wakati Mheshimiwa Rais, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli analihutubia Bunge hili wakati wa ufunguzi wake alisema asingependa tena kusikia tena hili neno la upembuzi yakinifu likiendelea kutumika kwa sababu linaonesha ni ambalo limekuwa liki-roll on mambo yaani ni utaratibu tu wa kutaka kuchelewesha. Sasa tunafahamu Serikali ina mipango yake na hapa unasema specifically kwamba itafanyika kwenye Mwaka wa Fedha 2019/2020. Sasa je, Serikali iko tayari kutueleza ni lini specifically mradi huu utaanza kufanyika ili kuondoa kero ya watu wa Liwale? Swali langu la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, ni kwamba matatizo yaliyoko Liwale yanafanana kabisa na matatizo yaliyoko Jimbo la Ndanda hasa kwenye Kata ya Nanganga. Kata ya Nanganga kuna mradi ambao ulikusudiwa upeleke maji kwenye vijiji vya Chinyanyila, Nanganga A na B, Mkwera moja na Mbili pamoja na Mumburu 1 na 2 pamoja na vijiji vya Chipite. Mpaka sasa hivi tunaonge ahapa mradi ule ulitekelezwa chini ya kiwango na inasemekana kwamba mkandarasi amekimbia hajaukamilisha na hajaukabidhi kufanya commissioning kama ambavyo ilikusudiwa.

Sasa nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, yuko tayari kupeleka wataalam wake kutoka Makao Makuu ya Wizara ya Maji wakauchunguze mradi huu na kutoa majibu stahiki kwa wananchi wale?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kumjibu Mheshimiwa Mbunge, moja; Wizara yetu ya Maji jukumu lake ni kuhakikisha Watanzania wanapata maji safi na salama lakini katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji katika Mji huu wa Liwale, kuna miradi ambayo inaendelea. Moja, mradi wa Kipure pamoja na Mangilikiti na Nanyungu yote ni katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji na hata katika bajeti hii yetu ya 2019/2020 tumetenga zaidi ya 699,000,000 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Kubwa, Mhandisi wa Mkoa, wahandisi wa wilaya wahakikishe fedha hizi zinatumika kuweza kutatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu mradi ambao ameuelezea nataka nimhakikishuie, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kutuma wataalam kwenda kuukagua mradi huo na mimi kama Naibu Waziri niko tayari kuongozana na wewe katika kuhakikisha tunaenda kuchukua hatua nzitio. Ahsante.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, naomba kuuliza swali la nyongeza, Korogwe Mji tuna kijiji kinaitwa Mahenge, kiko nje kabisa ya Mji wa Korogwe na katika mpango wa miji 28, sina hakika kama kinaweza kikafikiwa na ule mradi wa maji.

Je, mtakuwa tayari kukipatia maji kijiji hicho kwa kuwapa kisima cha maji kirefu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge anafanya kazi kubwa sana katika Jimbo lake wala haina haja ya kulalamika sana kwa sababu ukimuona mtu mzima ujue kuna jambo. Labda tuwaagize watu wa DDCI waende kuchimba kisima haraka pale ili wananchi wake waweze kupata maji safi na salama.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika mradi wa kutafuta chanzo cha pili cha mbadala cha maji ya Wilaya ya Liwale palitolewa shilingi milioni 300 na DDCIA walishaanza kufanya kazi hiyo lakini wamechimba visima viwili ambavyo vina uwezo wa kutoa maji lita 5,000 lakini visima vile vimetelekezwa mpaka leo.

Je, Serikali iko tayari kutoa fedha kwa ajili ya kwenda kufanya uendelezaji wa visima vile ambavyo viko katika Kijiji cha Makata na kijiji na Mikunya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza labda kwa nia njema kaisa katika kuhakikisha visima hivi vinakuwa endelevu labda baada ya saa saba nikutane na Mheshimiwa Mbunge na tuweze kufanya mawasiliano na wenzetu ili tangalie ni namna gani tunaweza tukasaidiana naye. Ahsante sana.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri alifanya ziara katika Mji wa Ruaha Mbuyuni baada ya kuonekana kuna shida kubwa sana ya maji na kipindupindu kinatokea kila mara na akaahidi pale kwamba kichimbwe kisima kwa tahadhari ili wananchi waanze kupata maji. Lakini kwa masikitiko makubwa wale wataalam wamepuuzwa hakuna aliyefika pale. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri atakubali tena kwenda kuona hali ilivyo na wananchi wanazidi kuteseka?

Swali la pili, kwa kuwa Serikali kuna wahisani ambao huwa wanansaidia Serikali, kuna tatizo kubwa katika Kijiji cha Udekwa na Mlafu, tayari Serikali ya Italy, kupitia Shirika linaitwa WAMAKI liko tayari kusaidia, lakini linataka commitment ya Serikali, yenyewe litasaidia kiasi gani, ili na wao waweze kusaidia fedha. Je, Serikali sasa itakuwa tayari kusaidia ili WAMAKI waweze kutoa maji safi na salama kwa kata mbili.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kabisa nilifika Kilolo na nimeona kazi nzuri ambayo inafanywa na Mheshimiwa Mbunge Venance Mwamoto katika Jimbo lake. Lakini kikubwa tulifika kweli Ruaha Mbuyuni na tukaona changamoto ile na tukatoa agizo, watu wa Bonde walikwenda walishafanya tafiti ya upatikanaji wa maji. Labda nimuagize sasa Mhandisi wa Mkoa, ahakikishe kabisa kile kisima kinachimbwa ili wananchi wale waweze kupata maji na anipatie taarifa.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu suala lake la pili, pamoja Serikali imekuwa ikitatua tatizo la maji, imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Serikali tupo tayari kukaa nao, tuangalie ni namna gani tunaweza tukashirikiana katika kuhakikisha tunatatua changamoto hii. Ahsante sana.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 11 Aprili, 2019 kwa kuwa Waziri aliapa mbele ya wananchi wangu na mbele ya Rais alipokuja tarehe hiyo. Je, ni lini mradi huu utaanza na ni mwezi gani utaanza ili wananchi wangu waendelee kuwa na imani kutokana na kiapo alichokifanya siku ile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, siku ile kulikuwa na changamoto ya Mradi wa Ngamanga, kwa kuwa siku ile ilionekana ni lazima wataalam wabaki pale ili waweze kutatua tatizo hili; ni lini sasa hatua zilizochukuliwa ili kutatua mradi huu wa Ngamanga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Sanga kwa kazi kubwa sana anayoifanya katika Jimbo lake la Makambako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kabisa Mheshimiwa Rais alivyofanya ziara na Mheshimiwa Waziri wetu alitoa commitment ya kuhakikisha mradi huu utatekelezeka haraka. Nataka nimtoe hofu kabisa sisi kama Wizara tumejipanga na tunatambua kabisa agizo la Mheshimiwa Rais kwamba tukishindwa kutekeleza mradi huu, tutatumbuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara ya Maji hatupo tayari kutumbuliwa, tutafanya kuusaini mkataba ule haraka ili utekelezaji wa miradi ya maji miji hii 28 utekelezwe kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa katika mradi ule wa Ngamanga, tulishatuma wataalam wetu na tumeshaangiza mabomba, kuna kazi inaendelea naamini ndani ya muda mfupi utakamilika na wananchi wake watapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mji wa Muheza ni mojawapo ya sehemu ambazo zitafaidika na mradi huu kutoka India. Vile vile wakati wananchi wa Muheza wanasubiri mradi huu ambao ni mkubwa, upo mradi mwingine wa kutoa maji katika Mji wa Pongwe na kuleta Muheza Mjini. Mradi huu umefikia asilimia 70 na tumebakiza asilimia 30 tu ili wananchi wa Muheza waanze kupata maji ya uhakika. Tatizo ni uchakavu wa mabomba ambayo yako pale Mjini Muheza. Nataka kujua, ni lini Serikali itaruhusu mabomba yale yaanze kufumuliwa na kazi hiyo ianze kufanyika ili maji hayo yaweze kuunganishwa kuja Mjini Muheza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa
Mbunge, amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana, hususan katika suala zima la utatuzi wa maji katika Jimbo lake la Muheza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Balozi Adadi ameshakutana na Mheshimiwa Waziri na tumeshakubaliana kwamba sasa ile kazi ya kuhakikisha tunaondoa yale mabomba inafanyika mara moja. Nami kama Naibu Waziri tutalisimamia katika kuhakikisha ile kazi inaanza na wananchi wake waweze kupata maji safi.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuuliza, ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa kuboresha upatikanaji wa maji katika Jimbo la Rombo kadiri ya mpango ambao tumeupeleka Wizarani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nampongeza Mheshimiwa Mbunge, amekuwa akiuliza swali la Rombo mara kwa mara na tumeshakubaliana tutakwenda Rombo, lakini kikubwa tunashukuru kwanza Bunge lako Tukufu limetuidhinishia kiasi cha shilingi bilioni 610 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wa Rombo kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji wa mradi wa Mingumbi – Miteja ambao umekamilika, Kijiji cha Njia Nne ambacho kimepitiwa na mradi huo hakikupata maji: Je, Serikali sasa iko tayari kusambaza maji kwa Kijiji hiki cha Njia Nne ili kuondokana na tatizo la maji ambalo liko pale?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; mwaka 2017, Wakala wa Serikali (DDCA) ilifanya mkataba na Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kuchimba visima virefu 21, lakini mpaka sasa wamechimba visima vitatu tu katika vijiji 18. Sasa je, DDCA iko tayari kuchimba visima virefu hivyo, au nini sababu zilizowafanya DDCA wasichimbe visima virefu katika Vijiji vya Nampunga, Chumo, Mtondo wa Kimwaga, Nandembo, Kibata, Kinjumbi, Somanga na Marendego?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anafahamu nia ya Serikali yetu. Zaidi ya shilingi bilioni 4,668 ziliwekezwa pale katika kuhakikisha tunatekeleza Mradi wa Maji wa Mingumbi na Miteja katika jitihada za kutatua tatizo la maji. Nataka nimhakikishie kwamba nia ya Wizara yetu ni kuhakikisha Watanzania wanapata maji safi na salama. Tutafanya extension ili wa Kijiji kile cha Njia Nne nao waweze kupata maji safi na salama katika kuhakikisha tunamtua mwana mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la uchimbaji wa visima, tulitenga kiasi cha shilingi milioni 456 katika kuhakikisha zaidi ya vijiji 19, ikiwa Kilwa Kusini na Kilwa Kaskazini vinapata huduma ya maji. Tuliwapa kazi hiyo DDCA, wamefanya kazi, lakini kulikuwa kuna ucheleweshaji mkubwa. Sisi kama viongozi wa Wizara tumeshamwondoa Mkurugenzi yule wa DDCA maana yake kulikuwa na ucheleweshaji. Yote hii ni kuweka mtendaji ambaye ataendana na kasi ya kuhakikisha tunatatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Ngombale, sisi kama Wizara ya Maji tutahakikisha kwamba visima vilivyobaki vinachimbwa kwa wakati na wananchi wake waweze kupata maji safi na salama.
MHE. SELEMANI S. BUNGARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu hayo kuhusu Wilaya ya Kilwa, lakini Wilaya ya Kilwa kwenye Hospitali ya Wilaya kuna uhaba mkubwa wa maji: Je, Serikali inatuambia nini kuhusu jambo hili la Hospitali ya Wilaya kupata maji ya uhakika na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, sisi kama Serikali na Mheshimiwa Mbunge anatambua, ni miongoni mwa jitihada ambazo tunazifanya katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji katika Jimbo lake la Kilwa Kusini. Yupo katika mpango wa miji 28, lakini kama unavyotambua, suala la hospitali ni suala la dharura sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikubaliane na Mheshimiwa Bungara tukutane baada ya saa saba ili tuwasiliane na wataalam wetu tuangalie ni namna gani tunaweza tukawapatia wananchi wake huduma haraka katika suala zima la maji.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali moja na nyongeza. Kwa kuwa Serikali ilikuwa na mpango wa kuchimba visima vya maji katika Vijiji vya Ng’hambi, Kiegea, Kazania na Chimaligo; na fedha zilitengwa, visima havijachimbwa? Mheshimiwa Waziri unaweza kuwaeleza wananchi wa vijiji hivyo fedha hizo zilikwenda wapi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge. Kiukweli amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana katika suala zima la maji. Ukimwona mtu mzima analia, ujue kuna jambo Mpwapwa. Sasa nataka nimhakikishie, kwanza nipo tayari kwenda Mpwapwa, lakini kuzifuatilia hizi fedha katika kuhakikisha zinafanya kazi na wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa utekelezaji wa miradi ya maji unategemea na mpango wa fedha, natambua kuna baadhi ya Wakandarasi bado hawajalipwa fedha zao: Je, ni lini sasa Mkandarasi ambaye anatekeleza mradi wa Mji Mdogo wa Ilula katika Jimbo la Kilolo atapatiwa malipo yake ili wananchi wa Ilula waache kupatiwa migao ya maji mara kwa mara?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwapigania akina mama na Watanzania hususan katika suala zima la maji. Kikubwa, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Kama unavyoona, gari haliwezi kwenda bila mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tulikuwa tunadaiwa takribani zaidi ya shilingi bilioni 88 na Wakandarasi, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na Wizara ya Fedha, wametupatia fedha zote shilingi bilioni 88 ambazo tulikuwa tunadaiwa na Wakandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, katika mradi wake ule wa Ilula kwa Mheshimiwa Mwamoto, Kilolo pale, tumeshamlipa zaidi ya shilingi bilioni moja. Tunataka zile fedha tulizomlipa sasa awekeze pale katika kuhakikisha anakamilisha mradi na wananchi wa Ilula waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatolesheleza.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, sasa Serikali imetenga pesa kama ilivyo katika majibu ya msingi. Na kwa kuwa, tatizo la maji katika Kata zilizotajwa katika swali hilo ni ya muda mrefu. Je, Serikali inaji-commit vipi kwamba, huu mradi wa kuweka maji katika kata hizo utakamilika wakati gani?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili ni kwamba, kumekuwa na matatizo makubwa sana katika miradi ya maji katika nchi yetu na Serikali inaahidi kutoa pesa kwenye bajeti, lakini fedha haziendi kama inavyotarajiwa, lakini pia hata fedha zinazoenda zinatumika vibaya na kuifanya miradi hii isikamilike. Je, Serikali sasa inachukua hatua zipi kuhakikisha kwamba, hii miradi ya maji ambayo inapata fedha za Serikali inakamilika na fedha zinatumika ipasavyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, nataka nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwanza sisi kama Serikali tumefanya jitihada kubwa sana pale Mikumi Mjini. Zaidi ya mradi wa milioni 974 tumeweza kutekeleza kupitia chanzo cha Madibira katika kuhakikisha wananchi wale wanapata huduma ya maji, lakini katika kuhakikisha tunatumia chanzo hiki cha Sigaleti sisi tunapitia usanifu kwa mara ya mwisho kabisa. Na ninataka nimhakikishie sisi kama Wizara ya Maji tutafanya jitihada kuhakikisha mradi huu tunauanza na kutekeleza katika kuhakikisha azma ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kumtua mwanamama ndoo kichwani inatimilika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili; utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Na sisi kama Serikali, Serikali inatupa fedha moja ya changamoto kubwa ilikuwa ni muundo, lakini kupitia Bunge lako Tukufu umetunga sheria katika kuhakikisha kwamba, tuna sheria Namba 5 ya Huduma ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira na Uanzishwaji wa Wakala wa Maji RUWASA. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge huu utakuwa muarobaini katika kuhakikisha usimamizi wa miradi ya maji na fedha, kwa maana ya wakandarasi katika kuhakikisha wanatekeleza miradi ya viwango na katika kuhakikisha tunatatua matatizo ya maji, ahsante sana.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunijalia kuingia kwenye Bunge lako Tukufu na kuweza kuwawakilisha ipasavyo Wananchi wa Jimbo la Singida Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Ikungi pamoja na Jimbo la Singida Mashariki ni kama ambavyo swali la msingi lilivyouliza lina matatizo yanayofanana na jimbo lililoulizwa katika swali la msingi. Pamoja na matatizo hayo zimefanyika jitihada, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya kipenzi chetu Dkt. John Pombe Magufuli, wameshatuletea takribani bilioni 1 na milioni 500 kuchimba visima virefu 28.

Mheshimiwa Spika, sasa nimekuja hapa kuomba kwa kupitia Waziri, wako tayari, tumeshafanya tathmini ya kutosha tuweze kupata, maana kuchimba maji na kuyapata ni jambo moja na kutoka maji ni jambo la pili. Kwa hiyo, ninaomba Mheshimiwa Waziri anihakikishie kwamba, kupitia tathmini iliyofanyika na iko Wizarani tunahitaji jumla ya bilioni 2 ili tuweze kutengeneza miundombinu ya maji Wananchi wa Singida wapate maji. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kwanza namfahamu vizuri alikuwa Mkuu wa Wilaya, lakini nataka niwahakikishie wana-Singida Mashariki hili ni jembe wembe walitumie vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, katika kuhakikisha kwamba, tunatatua tatizo hili la maji tumeshafanya jitihada za uchimbaji. Nimuombe baada ya Bunge Saa saba tukutane tupange mikakati ya kwenda kutatua tatizo la maji kwa haraka kabisa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba niulize maswali yangu mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwanza Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Spika wewe ni shahidi, huu mradi ni wa muda mrefu sana zaidi ya miaka 11. Miaka mitatu mizima tunazungumzia suala la chujio, si sawa kwa wananchi wa Bunda na Mkoa wa Mara. Naomba niulize maswali yangu mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, mbali na changamoto za wakandarasi kutokulipwa, mbali na changamoto za wakandarasi kuondoka site, Mamlaka ya Maji ya Mji wa Bunda kupitia vyanzo vyake vya ndani vimeanza kusambaza mitandao ya maji. Sasa nilitaka kujua Serikali mna mkakati gani wa kusaidia jitihada hizi za mamlaka ya maji Mji wa Bunda mbali na kwamba, haipati ruzuku Serikalini, kuendelea na zoezi la usambazaji wa miundombinu ya maji katika maeneo mbalimbali ikiwepo Manyamanyama, Bunda Store, Gerezani, Olimpas, Sazila; Serikali lini mtahakikisha hii mitandao ya maji yanafika kwenye maeneo hayo ambayo hakuna kabisa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Mheshimiwa Naibu Waziri unajua Mamlaka ya Mji wa Bunda, Halmashauri yetu ya Mji wa Bunda ni Mpya. Tumekuta kuna madeni ya umeme ambayo mwisho wa siku takribani milioni 603 hayo tumerithi. Mamlaka yangu ya Mji wa Bunda inalipa bili current bili inalipwa, lakini haya madeni yamerithiwa kupitia halmashauri iliyopita tangu Mzee wangu Wassira. Wizara mna mkakati gani kuhakikisha hli deni linalipwa, ili umeme usikatwe wananchi waweze kupata huduma ya maji maana wao ndio wanaoathirika na bili inalipwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, cha kwanza nataka nikiri kwamba, moja ya changamoto kweli tuliyokuwanayo ilikuwa wakandarasi wababaishaji, lakini uanzishwaji wa RUWASA mmekwishatupa rungu sisi viongozi wa Wizara ya Maji, hatuna sababu hata moja ya kulalamika. Tutachukua hatua kwa mkandarasi yeyote ambaye atataka kutuchelewesha katika kukamilisha miradi yetu ya maji.

Mheshimiwa Spika, kikubwa kutokana na mradi ule Mheshimiwa Waziri amekwishatoa agizo kwamba, mradi ule sasa tutatekeleza kupitia wataalam wetu wa ndani katika kuhakikisha tunawapa uwezo Mamlaka ile ya Bunda kwamba, tutatoa milioni 375 na wataalam wetu wa ndani wataukamilisha mradi ule kwa haraka. Na kazi iliyobaki ni wataalam wetu wa mamlaka sasa kuwaunganishia wateja wao, ili waweze kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala zima la ukatikaji wa umeme na madeni yaliyopo, hii ni Grade C mamlaka yao. Sisi kama Wizara yetu ya maji tumeona haja sasa ya wao kulipa kidogo na sisi tuweze kuwaongezea ili katika kuhakikisha tunakamilisha deni lile na wananchi wa Bunda waendelee kupata huduma ya maji. Pia natambua kwa Mheshimiwa Kangi Lugola kukamilika kwa mradi huu maeneo ya vijiji jirani kwa maana ya Buzingwe, Bulamba na Kabainja nao watapata huduma ya maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Esther Bulaya kukamilika kwa mradi huu utafanya maamuzi sahihi sasa ya kurudi nyumbani, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa niwashukuru Wizara ya Maji kwa sasa kwa kweli tuseme ukweli kwamba, viongozi wote Mawaziri, Makatibu na watendaji wote sasa wako kazini, wanafanya kazi vizuri, niwashukuru sana. Katika Jimbo la Bunda wataalam walifanya tathmini ya kuchimba visima vya maji ikaonekana kwamba, visima vinakauka, Wizara ikaja na mkakati wa kuchimba malambo zaidi ya malambo 16 ambayo ni matumizi ya maji, sasa kwa mwaka huu wamechagua kuchimba malambo matano. Nilitaka kuuliza tu Waziri, ni lini sasa haya malambo matano yatafanyiwa kazi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kiukweli anafanya kazi kubwa sana. Jana tu tulikuwepo nae katika Wizara yetu ya maji na Katibu Mkuu na moja ya makubaliano ni katika kuhakikisha tunatia fedha kwa ajili ya uchimbaji wa mabwawa zaidi ya matano. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nataka nikuhakikishie sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa Wananchi wako wa Bunda Vijijini kuweza kuchimbiwa mabwawa haya na waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, pia, nitumie nafasi hii kuwapongeza Wabunge wa Mkoa wa Mara wanaotokana na Chama cha Mapinduzi kwa mshikamano wao na kuweza kupigana. Zaidi ya miradi Mgango, Kyabakari tumekwishasaini, lakini tunakwenda kutatua tatizo la maji Mugumu pamoja na Tarime. Ahsante sana.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, ahsante ningependa kuuliza swali moja la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Vijijini tumechimbiwa visima 11 na kati ya visima hivyo, visima vitatu tayari Serikali imeridhia mchakato wa kutafuta mkandarasi uanze.

Je, ni lini Serikali itaridhia na visima vinane vilivyobaki navyo mchakato wa kutafuta mkandarasi uanze, ili huduma ya upatikanaji wa maji Jimbo la Mtwara Vijijini iboreke?

SPIKA: Majibu ya swali hilo Mheshimiwa Naibu Waziri Maji, tafadhali.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, lakini la kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, mama yangu Hawa, kwa kazi kubwa anayofanya katika jimbo lake, lakini kikubwa nimuagize Mhandisi wa Mkoa kwa maana ya Meneja wa RUWASA katika kuhakikisha analifuatilia hili jambo na ahakikishe lianze kwa haraka. Na sisi kama Wizara ya Maji tupo tayari kuwapa msaada, ili mradi huu uanze kuwaka kwa wakati.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Matumizi ya maji ya Ziwa Chala yaliombwa hapa Bungeni na Wabunge wote walionitangulia; Mheshimiwa Alphonce Maskini, Mheshimiwa Aloyce Ngalai, Mheshimiwa Justine Sarakana, Mheshimiwa Basil Pesambili Mramba na Awamu zote Tano za utawala wa nchi hii. Naomba nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano na kuishukuru kwa uamuzi wake wa kuamua kutumia maji haya kwa ajili ya wananchi wa Rombo na nina hakika kama mradi huu utatekelezwa shida ya maji katika Jimbo la Rombo itakuwa ni historia. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, sasa ningependa kuuliza mradi huu unategemewa kuanza na kumalizika lini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hivi sasa kuna visima viwili ambavyo vimeshakamilika vinatusumbua sana pale Rombo, Kisima cha Leto na Kisima cha Shimbi Mashariki. Namshukuru Naibu Waziri, wiki iliyopita alikuwa Rombo na alitoa maagizo ili haya maji yapate kutumika kwa wananchi.

Sasa swali langu maagizo yamekuwa yanatolewa lakini hayatekelezwi, je, sasa Serikali iko tayari kuwashughulikia maofisa na watendaji ambao wanazuia maji haya yasitumike na kusababisha mateso kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli uungwana ni vitendo Mheshimiwa Mbunge ni muungwana. Kutokana na uungwana huo wa kushukuru sisi kama Serikali nataka nimhakikishie tutatekeleza Mradi ule wa Ziwa Chala katika kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo la maji na mpaka hivi tunavyozungumza tulishatoa agizo kwa maana ya wataalam wetu waweze kufanya makisio na tutawatumia shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya uanzaji wa mradi ule ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, la pili nikiri kabisa tuna Mradi wa Leto pamoja na Shimbi Mashariki, nimetoka juzi, moja ya changamoto ulikuwa ni uzembe wa mkandarasi ilihali fedha tumempa. Kwa hiyo tumemwagiza na tumemshughulikia ipasavyo, ndani ya wiki hii maji yale yatafunguliwa na wananchi wako wataweza kupata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, pamoja na shukurani za dhati kutoka kwa wananchi wa Wilaya ya Misenyi na Jimbo la Nkenge kwa mradi mkubwa wa maji ambao kwa mara ya kwanza sasa unaanza kutekelezwa, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; pamoja na ukweli kwamba mradi huu ni mkubwa lakini majibu yanaonyesha utatekelezwa katika bajeti ya Mwaka 2019/2020. Sasa katika kipindi hiki ambacho wananchi wanasubiri mradi huo mkubwa nini Serikali inafanya kuhakikisha maji yanaendelea kupatikana kwa uhakika ili wasipate tabu wakati wakisubiri mradi mkubwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili dogo; katika kikao changu cha wadau, wataalam waliniandalia taarifa nzuri na nikawaeleza wadau kuhusu Mradi wa aji ya Ruzinga lakini wadau wengi wakasema hapana Mheshimiwa unadanganywa, maji Ruzinga hayatoi.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kufuatana na mimi ili twende kati ya Ruzinga ili tuone hizi fedha nyingi tunazopeleka tunafikiri maji yanatoka na hayatoki ili isije ikafika wakati mwingine ambao siyo muafaka wa kuuliza maswali kama haya twende pamoja anisaidie kutoa maelekezo ya Muarobaini wa matatizo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli amekuwa akifanya kazi kubwa sana katika Jimbo lake. Kitu ambacho nimhakikishie; mimi ni Naibu Waziri wa Maji, faraja yangu ni kuona Wanankenge wanapata maji safi na salama. Sasa nataka nimhakikishie baada ya Bunge tutafika na tukiona mradi ule ambao tumetoa fedha maji hayatoki tutamchukulia hatua Mhandisi wa maji pamoja na Mkandarasi ambae amepewa sehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa ambacho nataka kumweleza Mheshimiwa Mbunge ahadi ya utekelezaji wa mradi mkubwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na watalaam wetu wameshafanya usanifu ninachotaka kumhakikishia, katika kipindi hiki ili wananchi waweze kupata huduma ya maji timu yetu imegundua kisima kikubwa sana katika Kijiji cha Igayaza, tutatekeleza mradi wa haraka ili wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu sana ya maji. Maji ni uhai na sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatupo tayari kupoteza uhai wa Wanakyaka. Ahsante sana.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa matatizo wanayoyapata wananchi wa Nkenge pia yanawapata wananchi wa Kigamboni. Je, Serikali ina mkakati gani mahususi wa kuhakikisha chanzo cha maji cha visima vya Kimbiji na Mpera kinakamilika ili wananchi wa Kigamboni, Mbagala, Chamazi, Temeke na maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwa ufupi, hii ni Serikali ya Awamu ya Tano ikiahidi inatekeleza. Tumeshachimba visima zaidi ya 20 katika Kimbiji na Mpera na mpaka sasa tumeshamkabishi Mkandarasi kwa ajili ya uanzaji wa mradi wa Kigamboni ili wananchi wa Kigamboni waweze kupata huduma ya haraka. Kikubwa ambacho tunachotaka kumsisitiza Mkandarasi wa mradi ule aweze kufanyakazi kwa mujibu wa mkataba ili uweze kukamilika kwa wakati na wananchi wa Kigamboni na maeneo mengine waweze kupata huduma ya maji. Ahsante sana.
MHE. ESTHER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba niulize swali dogo la nyongeza. Najua mradi wa Maji Bunda ni wa muda mrefu na nimeushughulikia sana, hilo halina ubishi. Najua tatizo sasa hivi siyo maji kutoka kwenye chanzo kule Nyabehu, tayari sasa hivi maji yanakuja. Tatizo kubwa ni mtandao wa kuhakikisha wananchi wengi wa Bunda Mjini wapate maji safi na salama. Sasa, ni lini Serikali watahakikisha wanasambaza mtandao mkubwa wa maji na kuunga mkono juhudi zangu kwa kutenga fedha za Mfuko wa Jimbo kuwasaidia kutandaza huo mtandao ili wananchi wa Bunda kwenye kata zote 14 wapate maji safi na salama, ni lini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Bulaya kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda atambue kwamba Serikali imefanya jitihada kubwa sana katika Jimbo lake la Bunda, tuna utekelezaji wa mradi zaidi ya bilioni 10, huo unaendana sambamba kabisa na utandazaji wa mtandao wa maji. Kikubwa ambacho ninachotaka kumhakikishia, Serikali hii ya Awamu ya Tano tutahakikisha kazi ile inakamilika kwa wakati na wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu sana ya maji.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri Mradi wa Maji wa Kata ya Sigino, Mheshimiwa Waziri alifika mwaka jana akaahidi kwamba wataalam wake watafika ndani ya siku 10 ili ule mradi uanze.

Naomba nifahamu hawa watalaam watafika ili wananchi wale wapate maji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya tukutane basi baada ya Bunge ili tuweze kukutana na wataalam wetu na kuweza kuwaagiza haraka wafanye kazi. Ahsante sana.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba niishukuru sana Serikali kwa majibu yake mazuri hasa kukamilisha angalau kupeleka maji katika Wilaya ya Magu pale Magu Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu; kwa sababu muuliza swali la msingi amezungumzia vijiji kadhaa ikiwemo pamoja na Kijiji cha Kabila ambacho kina wakazi wengi sana. Ili kuondoa tatizo la ukosefu wa maji na Mheshimiwa Waziri anajua kabisa kwamba maji ni uhai, ni lini sasa angalau kwa kuanzia kabla ya Mradi mkubwa huu wa Maji ya Ziwa Victoria haujaanza angalau kwenda kufufua vile visima ambavyo vilikuwepo kama ambavyo tunavyofanya sasa kwenye eneo la Jimbo la Sumve pamoja na Magu, lakini pia kusafisha vile visima ambavyo vilikuwa vinafanya kazi. Sasa Serikali kwa nini sasa isifanye utaratibu wa kuchimba na kusafisha vile visima ambavyo vilikuwepo? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndassa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mzee wangu, Mzee Ndassa sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji tumeainisha Mikoa zaidi ya 17 yenye changamoto ya maji ikiwemo eneo la Mkoa wa Mwanza, lakini tumepata fedha kutokea World Bank na katika Mikoa hii 17 tumepeleka kila Halmashauri 1.3 billion ikiwemo katika Jimbo lake la Sumve.

Nimwombe sana Mhandisi wa maji akae na Mheshimiwa Mbunge na mimi mwenyewe nipo tayari ili katika kuhakikisha fedha zile zinaelekezwa katika zile changamoto ambazo Mheshimiwa Mbunge amezianisha. Ahsante sana.
MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Katika Jimbo la Bunda Vijijini kuna Mradi wa Maji Nyamuswa na kuna Mradi wa Maji Mgeta na Naibu Waziri ailifika kwenye maeneo hayo lakini mpaka sasa ile Kamati aliyoiunda kufuatilia shughuli hizo haijakwenda vizuri.

Je, Naibu Waziri yuko tayari sasa kushughulika na hilo jambo ili watu wa Nyamuswa na Mradi wa Mgeta-Nyangarangu wapate maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipo tayari. Ahsante sana.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Pamoja na shukurani za wananchi wa Jimbo la Mtama kwa miradi kadhaa inayoendelea ya maji katika Jimbo hilo baada ya Mji wa Mtama kupewa hadhi sasa ya kuwa Halmashauri mahitaji ya maji yameongezeka sana katika Mji huu. Je, Serikali sasa iko tayari kwenye bajeti ya mwaka huu kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu na upatikanaji wa maji katika Mji huu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, Kaka yangu Mheshimiwa Nape.

Mheshimiwa Nape anafanya kazi kubwa na nzuri na alishakuja katika Ofisi yetu ya Wizara ya Maji, tukakaa mimi, yeye, Waziri pamoja na Katibu Mkuu. Hakuna haja ya kusubiri mpaka bajeti fedha tumekwishatuma 1.3 billion kwa ajili ya utekelezaji. Mheshimiwa Mbunge asimamie mradi ule uanze haraka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Mji wa Tunduma ni mji unaokua kwa kasi na kuna miradi karibuni miwili au mitatu inatekelezwa kwenye Mji wa Tunduma, lakini tangu imeanza kutekelezwa mpaka sasa hivi wananchi hawajaanza kupata maji ya uhakika na Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja wamekuwa wakiwapa tarehe kila wakati za kumaliza miradi hiyo.

Je, ni lini miradi hiyo itakamilika ili wananchi wangu wa Mji wa Tunduma waanze kupata maji safi na salama kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nashukuru kuona Mheshimiwa Mbunge anakiri kwamba tunafanya kazi kubwa na ipo miradi ambayo tunaitekeleza katika Jimbo lake. Kikubwa ambacho ninachotaka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama viongozi wa Wizara tumeshabainisha miradi ambayo ipo katika hatua mbalimbali kwa ajili ya ukamilishaji. Tumepanga katika wiki hii ya maji itakuwa siyo wiki ya mapambio, ni wiki kwa ajili ya kuzindua miradi yote ya maji, kwa hiyo Wakandarasi wajipange katika kuhakikisha wana-meet zile commitment tulizoziweka ili wiki hii ya maji tuweze kuzindua miradi mingi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunakualika katika kuzindua miradi yetu ya maji. Ahsante sana.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza, naomba nitoe kwa dhati kabisa shukrani kubwa kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa miradi mingi aliyoweka katika Jimbo langu. Naomba niitaje hapa kwa niaba ya Bunge ili lielewe miradi gani ipo Jimboni kwangu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria ambao ni sehemu ya shilingi bilioni 600; Kituo cha Afya cha Upuge, shilingi milioni 850; Hospitali ya ngazi ya Wilaya Isikizye shilingi bilioni mbili; Kituo cha VETA kinachojengwa Isikizye, sasa ni shilingi bilioni tano; Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Magharibi mabilioni na umeme wa REA wa vijiji 18 mabilioni ya shilingi. Naomba salamu hizi na pongezi zimfikie Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Je Serikali ina mpango gani kupelekea maji vile vijiji 42 vilivyobakia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka wataalam wa maji ili kuchunguza vyanzo vya maji katika vijiji vya Kata za Ufuluma, Shitage, Nsimbo, Bukumbi, Makazi na Igulungu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri aliyekuja kufuatilia mradi huko kwetu, nasi tumemwekea binti aende akaoe. Karibu sana Mheshimiwa Aweso. (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, lakini nashukuru kwa zawadi aliyonipa. Nataka nimhakikishie mimi beberu, siyo jogoo la pasaka bwana, nipo tayari. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kama Serikali ambacho nataka kusema ni kwamba tumejipanga vizuri katika kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo la maji katika Mkoa wa Tabora. Tuna mradi mkubwa zaidi ya shilingi bilioni 600. Pamoja na hayo, kutokana na mapenzi makubwa na mahaba ya Mkoa wa Tabora, tumeshapeleka shilingi 8,345,000,000/= katika kuhakikisha tunaendelea kutatua tatizo la maji na fedha hizi tutatekeleza kwa kutumia wataalam wetu wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji tupo tayari kupeleka wataalam kufanya usanifu kwa vijiji ambavyo havijapata maji ili viendelee kupata huduma hii muhimu sana ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Waziri amesema kwamba mradi wa kutoka Nyahiti umekamilika, siyo kweli, nilikuwa huko juzi. Mradi huo hautoi maji na Mkandarasi hayuko site na hili lilikuwa ni agizo la Mheshimiwa Rais kwamba miradi kama hii yote ikamilike na ifanye kazi. Sasa atuambie, Wizara imekaidi agizo la Mheshimiwa Rais? Je, ni lini wananchi wa Misungwi watapata maji ya uhakika ? Ukizingatia wako karibu kabisa na Ziwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Mwishoni mwa mwaka 2019 Serikali iliweka miundmbinu katika Kata ya Shibula na Bugogwa katika Jimbo la Ilemela, lakini maji hayatoki na yakitoka yanakuwa yanatoka kwa kusuasua na pia yanatoka machafu sana…

SPIKA: Mheshimiwa Susanne unahutubia badala ya kuuliza swali.

MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Spika, najenga hoja.

SPIKA: Aaah, uliza swali.

MHE. SUSANNE P. MASELE: Mheshimiwa Spika, ni lini sasa wananchi wa maeneo hayo watapata maji ya uhakika ili waweze kufaidi miradi hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza napenda kumfahamisha ndani ya wiki mbili nilikuwa katika Jimbo la Misungwi, nilikuwa na Mheshimiwa Mbunge na tumefanya kazi kubwa. Changamoto iliyokuwepo pale ilikuwa ni Mkurugenzi wetu wa Maji. Tumemwondoa na mradi huu mkubwa utasimamiwa na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira MWAWASA katika kuongeza utendaji. Mradi umekamilika kwa zaidi ya shilingi bilioni 12 katika kuhakikisha wananchi wa Misungwi wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la Ilemela pamoja na Nyamagana yake tuna mradi zaidi ya bilioni 38 tunatekeleza katika kuhakikisha wananchi wa Nyamagana pamoja na Ilemela wanapata huduma ya maji na nilikuwepo na Waheshimiwa Wabunge na wanafanya kubwa na nzuri na tumemwagiza Mkandarasi, kabla ya mwezi wa Tatu mradi uwe umekamilika na tutakwenda kuuzindua katika wiki ya maji. Kama tulivyosema, wiki ya maji haitokuwa wiki ya mapambio, wiki ya maji itakuwa ni kazi ya kuzindua miradi mbalimbali ya maji ikiwemo na Nyamagana. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza, naipongeza sana Serikali kwa miradi mikubwa ya maji ambayo inatekelezwa kwenye Mkoa wa Mwanza likiwemo Jimbo la Nyamagana na hakika ikikamilika miradi hii itakuwa suluhisho kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu dogo la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri, tunao mradi kwenye Kata ya Lwanima wa ujenzi wa tenki la karibia lita 450,000. Ni takribani miaka mitatu sasa na changamoto ni malipo ya certificate ya mwisho hayajalipwa mpaka leo. Ni nini kauli ya Serikali kwa watu wa Lwanima ambao mradi huu na tenki hili lenye matoleo zaidi ya 17 katika kila Mtaa? Ni lini fedha hizi zitatoka ili wakazi wa Lwanima waweze kupata maji ya uhakika na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nipende kumpongeza na nithaminishe kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Mbunge katika Jimbo lake la Nyamagana, lakini kikubwa maji ni uhai. Ninachotaka kumhakikishia, sisi kama Viongozi wa Wizara hatutakuwa kikwazo kwa Wakandarasi ambao wamefanya kazi yao thabiti kabisa na yenye weledi kuhakikisha kwamba tunawalipa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie, katika mfuko huu tutalipa ili mradi ule ukamilike na wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu ya maji. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Wilaya ya Hanang ni moja yenye Wilaya yenye taabu sana ya maji, lakini naishukuru Serikali kwa kazi ambayo tayari imefanyika, lakini bado taabu iko pale pale.

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Visima alikuja kule na mashine ndogo akashindwa kuchimba visima. Je, Mheshimiwa Waziri anasemaje? Wakala huyu atarudi lini ili achimbe vile visima ambavyo tulikuwa tunajua watavichimba? Ahsante tena. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kiufupi tu nimwambie mama yangu kwamba, tutawatuma haraka ili kuhakikisha wanakwenda kuchimba visima hivi ili wananchi waweze kupata huduma ya maji, hususan Gehandu.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Pamoja na shughuli nyingi za maendeleo zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, wawekezaji wengi wameamua kuja Dodoma na Serikali yenyewe inakuja Dodoma na vyuo vikuu vingi vinajengwa Dodoma, hasa maeneo ya Nala; na kwa kuwa, maeneo ya pembezoni kama vile Bahi, Wilaya ya Chamwino na maeneo mengine yanahitaji maji kwa ajili ya wawekezaji, je, Serikali iko tayari kuhakikisha kwamba, hao wawekezaji na wananchi wanaozunguka maeneo hayo hawakosi maji kwa ajili ya matumizi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa, maji ya Ziwa Victoria yameshaletwa mpaka Nzega na kuna taarifa hayo maji yanakuja mpaka Igunga. Je, Serikali haioni kwamba, suluhu ya kudumu kwa ajili ya mahitaji ya Dodoma ni kuleta maji ya Ziwa Victoria ambayo yatasaidia pia Mkoa wa Singida na Dodoma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze mama yangu Mheshimiwa Felister Bura amekuwa mpiganaji mkubwa sana, hususan kwa changamoto ya maji katika Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, kikubwa ambacho nataka niwahakikishie wakazi wa Dodoma kupitia uongozi mahiri wa kiongozi wetu wa Wizara ya Maji, Profesa Makame Mbarawa, tumekwishaliona hilo. Moja kuwaagiza DUWASA katika kuhakikisha kwenye makusanyo yao ya ndani asilimia 30 wahakikishe wanachimba visima virefu maeneo ya pembezoni ili wananchi wa Dodoma waweze kupata huduma ya maji.

Pili, mpaka sasa tumekwishalipa fidia katika Bwawa la Farkwa kwa wananchi wale ili tuweze kujenga Bwawa la Farkwa. Katika kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo la maji katika Mkoa huu wa Dodoma tumeshaanza kuanzisha timu ya kufanya study ya namna gani ya kuanzisha standard gauge kubwa katika miradi yetu ya maji. Moja ni katika kuhakikisha tunaandaa standard gauge ya kuyatoa maji Ziwa Victoria hadi kuyaleta hapa Dodoma. Subira yavuta heri. Heri itapatikana katika kuhakikisha kwamba, Mradi wa Ziwa Victoria unafikisha maji hapa Dodoma. Ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wananchi wa Mji wa Tarime wameendelea kupata adha kubwa ya maji safi na salama na hasa upatikanaji wake. Kupitia Bunge hili nimeshauliza maswali mengi sana na kuchangia na Serikali ikaahidi kwamba, itatoa suluhisho la muda mfupi la kuchimba visima 23 kandokando ya Mji wa Tarime kuweza kuboresha Mradi wa Gamasara na Bwawa la Nyanduruma, lakini zaidi kwenye bajeti iliyopita waliahidi Mradi wa Ziwa Victoria ambao unatokana na mkopo kutoka India kwamba, unaenda kuanza ambao ni suluhisho la muda mrefu.

Sasa napenda kupata majibu kutoka kwa Naibu Waziri, ni lini sasa hii miradi yote inaenda kutengemaa ili wananchi wa Mji wa Tarime waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, dada yangu Esther Matiko kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tuna Mradi pale wa Gamasara ulikuwa ukifanya kazi kwa kusuasua, nilifika na tumechukua hatua kubwa ya kushughulikiana na yule mkandarasi. Wiki hii tunafunga pampu ili kuhakikisha wananchi wale wanapata huduma hii ya maji, lakini tunatambua kabisa Mkoa wa Mara ni maeneo yenye changamoto.

Mheshimiwa Spika, tumepata fedha takribani kwa mikoa 17 mmojawapo ukiwa Mkoa wa Mara na tumekwishatuma fedha zaidi ya Sh.8,345,000,000. Katika jimbo lake mpaka sasa tumekwishatuma pesa zaidi ya Sh.1,345,000,000, hizo fedha ni kwa ajili ya utekelezaji. Kwa hiyo, hizo fedha ziende zikatumike katika kuhakikisha zinachimba visima katika maeneo yenye changamoto ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, pia katika kuhakikisha tunatatua kabisa tatizo la maji Rorya pamoja na Tarime ni moja ya maeneo ambayo tumeyaweka katika miji 28 kupitia fedha za India. Tunasubiri kibali kutoka Exim Bank ili tuweze kutangaza tenda kwa ajili ya kuwapata wakandarasi na Mradi ule mkubwa wa kuyatoa maji Ziwa Victoria ili wananchi wa Tarime waweze kupata huduma ya maji. Ahsante sana.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwanza nianze kuipongeza Serikali na kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi ya maji katika Wilaya ya Mbeya.

Mheshimiwa Spika, pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa bajeti ya ziada ya shilingi bilioni 3.3 kwa ajili ya mradi wa maji uliotolewa kwa ajili ya Mji wa Mbalizi pamoja na Kata za Bonde la Songwe na Ilota. Pamoja na pongezi hizo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ni lini miradi ya maji itapelekwa kwenye Vijiji vya Ilembo, Santilia, Inyala pamoja na Ikukwa ambapo kunajengwa vituo vya kisasa vya afya na pia kuna Hospitali ya Wilaya?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini sasa Mradi wa Mbalizi utakamilika kuhakikisha wananchi wa Bonde la Songwe, Ilota na Mji Mdogo wa Mbalizi wanapata huduma ya maji ya uhakika? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayofanya katika Jimbo lake. Sisi kama viongozi wa Wizara, mimi pamoja na Waziri wangu tulishafika kule kuhakikisha Mradi wa Mbalizi wa kiasi cha shilingi bilioni 3 tunausimamia ili ukamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sasa hivi baadhi ya kazi zinafanywa na wataalam wetu wa ndani wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mbeya. Ndani ya mwezi Machi, mradi ule utakamilika na wananchi wa Mbalizi watapata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mradi katika Vijiji vya Santilia pamoja na Ilembo na Ikukwa tulipata fedha zaidi ya shilingi bilioni 25 za Lipa kwa Matokeo na wafadhili wa DFID na Kijiji hiki cha Santilia kipo. Sasa tupo katika hatua ya manunuzi kuhakikisha tunaukarabati mradi ule na wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu ya maji.

Mheshimiwa Spika, nachotaka kumhakikishia kwa Vijiji vya Ilembo na Ikupwa katika awamu hii inayokuja ya fedha za Lipa kwa Matokeo tutaviweka katika kuhakikisha nao wanapata huduma hii muhimu sana ya maji. Ahsante sana.
MHE. BUPE N. MWAKANG‟ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Kiongozi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa kazi kubwa ya kuweza kumtua mama ndoo kichwani. Serikali hii imewaza kutuliza hata ndoa za wanawake wa Tanzania, wameweza kutulia kwa sababu maji yanapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizi sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza;

(i) Wilaya ya Nkasi ina takribani ya vijiji 35 wanaoishi pembezoni mwa Ziwa Tanganyika, na wanatumia maji ya ziwa Tanganyika ambayo yanawasababishia kupata magonjwa mbalimbali ikiwemo kipindupindu na magonjwa ya kuhara. Sasa ni lini sasa Serikali itawajengea visima virefu ambavyo vitawasababisha wapate maji salama?

(ii) Wilaya ya Nkasi imegawanyika katika sehemu mbili, Nkasi Kusini na Nkasi Kaskazini. Naishuruku Serikali imeweza kujenga visima 9 ambavyo sasa hivi vinaendelea kujengwa, lakini bado Nkasi Kusini ambavyo havijajengwa visima takribani 7 ambavyo tuliomba kijiji cha Masolo, Kijiji cha Milindikwa, Malongwe, Sintali, Nkana na vijiji vingine bado havijachimbiwa visima.

Je, nili sasa Serikali itachimba visima hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge amekuwa mpiganaji mkubwa hususani kwa kina mama wa Mkoa wake wa Rukwa. Lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji hatuta kuwa kikwazo kwa Mkoa wa Rukwa na Nkasi katika kuhakisisha wanapata maji. Ziara ya Mheshimiwa Waziri katika Jimbo la Nkasi kwa Mheshimiwa Kessy alilia sana pale Mheshimiwa Mbunge na tumetoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa katika mji wa Kilando pamoja na Namanyele zaidi ya milioni tano kwa ajili ya miradi ile mikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepata fedha za PforF zaidi ya bilioni nne kwa Mkoa wa Rukwa, tumepeleka bilioni 1.3 katika Wilaya ya Nkasi katika kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo la maji. Naomba Waheshimiwa Wabunge waende kusimamia miradi ile katika kuhakikisha wakinamama wanaendelea kutua na ndoo kichwani na ndoa zao zinaendelea kuimarika. Ahsante sana.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Na ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kutembelea katika kijiji cha Mbesa aliahidi kisima kirefu amechimba, amekwenda kuangalia na sasa ameahidi kutoa milioni 200 kwa ajili ya kufanya ule mradi kukamilike vizuri. Vilevile tunawashukuru wafadhili wetu waliojenga visima 72 na wengine wamejenga visima 90 katika Jimbo la Tunduru Kusini. Na nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa mradi wa Mbesa, mradi wa Lukumbuli ambao ulikamika miaka mitatu iliyopita na mradi wa wanalasa ambao ulikamilika zaidi miaka 9 iliyopita haufanyi kazi kutokana na tatizo la kutumia mafuta ya diesel ambayo wananchi wameshindwa kutumia.

Je, Serikali ina mpango gani wa kufunga solar ili wananchi waweze kutumia kwa ukamilivu?

Kwa kuwa katika mradi wa Kijiji cha Mtina uliokamika mwaka moja uliopita umeshindwa kufanya kazi vizuri kutokana na panel solar zilizopo pale kutokutosheleza kusukuma maji kwa ajili ya kupeleka kwa wananchi.

Je, Serikali haioni haja yakuongeza solar panel katika mradi ule ili uweze kuhudumia wananchi wa Mtina ipasavyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli ni miongoni mwa Wabunge wanafanya kazi kubwa sana, na niseme hili ni baba lao kwa eneo la Tunduru Mungu akubariki sana. Lakini kikubwa ninachotaka kukisema watalamu wetu kwa maana ya WARUSA pamoja na wizara hawana kisingizio tena, utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha, tumepata fedha kwa mikoa 17 zaidi ya bilioni 119. Hata katika Jimbo lako la Tunduru tumeshapeleka bilioni 1.3 hizi fedha ni kwa ajili ya kwenda kutatua changamoto za miradi ya maji. Ni mtake mhandishi wa maji wa Tunduru Kusini katika kuhakikisha anatumia changamoto hizi ili kukarabati na wananchi wako waweze kupata huduma ya maji safi na salama na yenye kutosheleza. Ahsante sana.
MHE. AYSHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, Mradi wa Maji Kintinku Lusisile, ulianza kutekelezwa chini ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa mwaka 2012, lakini hadi sasa imepita miaka saba mradi huu haujakamilika. Je, Serikali inasema nini kutokukamilika kwa mradi huu kwa wakati?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, mojawapo ya tatizo kubwa la kutokukamilika kwa mradi huu ni ucheleweshwaji wa malipo, mpaka sasa tumepokea shilingi milioni 750 nje ya shilingi bilioni 2.2 tangu kusainiwa kwa mkataba tarehe 23 Mei, 2018. Nataka commitment ya Serikali ni lini mradi huu utakamilika? Wananchi wa Jimbo la Manyoni Mashariki wameteseka kwa muda mrefu, Mheshimiwa Naibu Waziri naomba unipe majibu, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, kiukweli ni miongoni mwa Wabunge ambao wamekuwa wakipigania hasa upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Singida. Na ninataka nimhakikishie moja ya changamoto kubwa sana tukiri ilikuwa ucheleweshaji wa kukamilika kwa miradi ya maji. Tunashukuru sana Bunge lako Tukufu kwa kutupa rungu la kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini, hatuna sababu hata moja sisi kama viongozi wa Wizara ya maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Wizara tumejipanga vizuri na wakala huu wa maji umejipanga vizuri. Tutahakikisha mradi ule tunaukamilisha kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kikubwa utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mwezi huu tunawapa fedha, si yeye tu hapo Manyoni, na hata kwa Mheshimiwa Massare katika mradi wake ule wa Itigi ambao unatekelezwa na Nangai tutatoa fedha katika kuhakikisha miradi hii ya maji inakamilika kwa wakati na Wananchi wa Manyoni waweze kupata huduma ya maji. Pia, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Lubeleje, jana alizungumza hapa eneo la Bulima na Iyoma na Mima wote nao tutaweza kuwapatia huduma ya maji, ahsante sana.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante kwa nafasi hii, katika Halmashauri ya Lushoto, Kata ya Manolo kuna mradi ambao umesainiwa tangu mwaka 2013, tunavyozungumza hadi sasa Serikali imeshalipa hela zote kwa mkandarasi, lakini jambo dogo la shilingi milioni 82 za VAT Serikali imeshindwa kuondoa na mpaka sasa hivi wananchi wale wanapata shida tangu mwezi wa sita mpaka sasa hivi shilingi milioni 82 imekuwa ni kikwazo cha Wananchi wa Manolo kupata maji safi na salama.

Je, Serikali inatoa kauli gani kwa Wananchi hawa wa Manolo ambao wanaendelea kuteseka kwa kukosa maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge. Kiukweli Mheshimiwa Shangazi mradi huu umeupigania sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya changamoto ilikuwa ni suala la fedha, mkandarasi alikuwa akidai takribani milioni 600 na sisi kama Wizara ya maji tulitengeneza commitment na tukamlipa ile fedha. Sasa hii changamoto ya VAT nataka nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge Serikali haijawahi kushindwa, sisi kama Wizara ya Maji tupo tayari tutakaa na Wizara ya Fedha haraka katika kuhakikisha changamoto hii tunaitatua kwa haraka, ili Wananchi wako waweze kupata huduma ya maji safi na salama, ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii:-

Mheshimiwa Naibu Spika naishukuru sana Serikali nilishawahi kuongea na Mheshimiwa Waziri kuhusu tatizo la maji katika Kata ya Magadu, wananchi wanapata matatizo kwa muda mrefu. Na chanzo cha maji kutokana na utafiti ni kuwa tayari kilishapatikana kutoa mbete. Je, kuna tatizo gani la kuendeleza hicho chanzo cha maji kuhusu Wananchi wa Magadu na mitaa mingine waweze kupata maji ya kutosha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kiukweli nimpongeze Mheshimiwa Mbunge amekuwa mfuatiliaji sana na ameshafanya kikao na Mheshimiwa Waziri. Nataka nimuombe basi baada ya Bunge tukutane na wataalam wetu tuangalie namna gani ya kuweza kuwasaidia Wananchi wa Magadu.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwanza napenda kumshukuru Naibu Waziri maana tarehe 07 Agosti, alikuja Wilaya ya Tarime na kuna maagizo aliyatoa kwenye Mradi wa Gamasara na wa Nyanduluma, lakini nataka kujua ni lini sasa vile visima 23 ambavyo Bunge lililopita niliuliza hapa na ukaelekeza kwamba, ni DCA wanaenda kuanza kuvichimba mara moja, lakini mpaka sasa hivi hamna chochote ambacho kinaendelea kwenye Jimbo la Tarime Mjini, ili kuweza kutoa suluhisho la la muda mfupi wakati tukisubiri ule mradi wa Ziwa Viktoria? Ahsante?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, nikiri nimefika Tarime na moja ya changamoto kubwa kiukweli changamoto kubwa ipo pale Tarime. Na moja ya changamoto ambayo tumeona jambo la kulifanya haraka kwanza tume-terminate mkataba wa yule mkandarasi wa Mradi wa Gamasara, mradi ule tutaufanya kwa sisi wenyewe kuwapatia fedha wataalam wetu waweze kuutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna suala la uchimbaji wa visima. Tumekwishawaagiza watu wa DDCA na sisi tumejipanga kuwapatia fedha ili uchimbaji wa visima 23 uweze kuchimbwa pale wakati tunasubiri mradi mkubwa wa fedha zile za India. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa wananchi wa Tarime kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu ya Serikali kuonyesha baadhi ya miradi ambayo inayofanyika katika Jimbo la Momba lakini bado tatizo la maji ni kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Maji inataka kwamba mwananchi achote maji umbali wa mita 400 na Jimbo la Momba lina zaidi ya vitongoji 400 na kiukweli mpaka sasa hivi tukienda katika level ya vitongoji peke yake vyenye maji haviwezi kufika hata 30. Kwa hiyo, nilichokuwa nataka kabla ya kwenda kwenye Uchaguzi Mkuu Serikali watupe hapa jibu la uhakika ni lini wananchi wa Momba maji yatatoka? Kwa sababu wananchi wanachohitaji pale ni maji pekee. Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, sisi kama Bunge hapa tuliitaka Serikali iongeze tozo kwenye mafuta kwa lengo moja tu la kupata fedha kwa ajili ya kupeleka kwenye miradi ya maji. Je, ni kwa nini ile tozo ambayo Bunge tuliipendekeza mpaka sasa Serikali haijaitekeleza? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai na sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji tunafanya jitihada kubwa sana za usiku na mchana katika kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji. Tumebainisha Mikoa 17 na Halmashauri 86 ambazo zimekuwa na changamoto kubwa sana ya maji ikiwemo Jimbo la Momba. Zaidi ya Sh.5,641,000,000 tumezipeleka kwenye Mkoa wa Songwe na katika Jimbo lake zaidi ya shilingi bilioni 1.3 zipo kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa mitano katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Azma ya Mheshimiwa Rais ni kumtua mwanamama ndoo kichwani, nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajipanga kuhakikisha miradi hii kwa wakati ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Serikali kutoa fedha nyingi sana, moja ya changamoto kubwa sana ya Wizara ya Maji ilikuwa katika suala zima la usimamizi wa miradi ya maji na uendeshaji. Miradi ilikuwa ikitekelezwa kwa gharama kubwa sana zaidi ya mfano wake. Mfano, ukienda katika Jimbo la Nkasi kulikuwa na mradi ambao unatekelezwa estimation yake ni shilingi bilioni 6 lakini Mheshimiwa Makame Mbarawa na timu ya Wizara imepitia na kugundua mradi ule unatakiwa kutelezwa kwa shilingi bilioni 3.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumeona kwamba pamoja na utekelezaji wa miradi lakini kwenye estimation za utekelezaji wa miradi zimekuwa kubwa sana. Sisi kama Wizara ya Maji tumepanga miradi yote kutekelezwa kwa Force Account kwa maana ya kutumia wataalam wetu wa ndani. Kwa hiyo, zile fedha ambazo tutakazopatiwa na Serikali zitatuwezesha kutekeleza miradi kwa wakati na tuta-save gharama kubwa sana. Kwa hiyo, nina imani fedha hizi zitaweza kutusaidia kutekeleza miradi mingi kwa kutumia wataalam wetu wa ndani na kuzuia ubadhirifu unaofanywa na wataalam wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. MENDARD L. KIGOLA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huu mradi wa maji wa Sawala umechukua muda mrefu sana zaidi ya miaka 6 na Serikali mara ya kwanza ilitoa fedha zaidi ya milioni 200 lakini hakuna kitu ambacho kimefanyika. Mara ya pili imetoa milioni 230, hakuna kitu kilichofanyika na wananchi pale sasa wanakata tamaa. Swali langu, ni lini mradi huu utakamilika ili wananchi waanze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna wakandarasi wawili wameshatolewa, sasa hivi Serikali inatumia mbinu gani ili kuhakikisha kwamba ile kazi inafanyika kikamilifu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuweza kufuatilia miradi yake ya maji. Kikubwa utekelezaji wa miradi ya maji katika ubora unategemeana na upatikanaji mzuri wa wakandarasi.

Mheshimiwa Spika, nilifika pale Mufindi Kusini eneo lile la Mtwango, moja ya changamoto kubwa mkandarasi ambaye amepewa kazi ile alikuwa wa kibabaishaji (kanjanja) kwa hiyo tulimuondoa mkandarasi yule lakini tumeiagiza TAKUKURU kuhakikisha fedha zile za wananchi walipakodi azitapike mkandarasi yule. Sisi kama wizara tumehukua jukumu sasa la kuwapatia ndugu zetu wa Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) kwa maana ya kufanya kazi ile kwa force account mradi ule ukamilike na wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Wizara ya Maji tunatumia forced account katika kuhakikisha mradi ule tunautekeleza kwa wakati na wananchi wako waweze kupata huduma hii muhimu. (Makofi)
MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Maeneo niliyosema ya Naisinyai na Mererani ni maeneo ambayo tunapata madini ya tanzanite, ni aibu sana kama pamoja na rasilimali hiyo kubwa maeneo yale hayana maji. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri anihakikishie kwamba bomba lile litakapopita Vijiji vya Lengasti, Mihiye, Oloshonyoke kama ambayo umesema yatapata maji.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna bomba la maji kutoka Ruvu kwenda Olekosmet la takribani bilioni 41, niishukuru Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuleta mradi huu. Je, yupo tayari kuongozana na mimi kukagua mradi huu ili ifikapo Mei mwakani kama ambavyo Serikali imeahidi mara zote mradi huu uweze kukamilika na wananchi wapate maji safi na salama kwa ajili ya mifugo na watu wa Simanjiro?. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya, kiukweli ni miongoni mwa Wabunge ambao wanafanya kazi kubwa sana na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge anatosha mpaka chenji inabaki.

Mheshimiwa Spika, kikubwa ambacho ninataka kukisema, tunatambua maji ni uhai na sisi kama Wizara ya Maji eneo lile la Mererani tulishachimba kisima kikubwa lakini changamoto ambayo tuliiona ni kuwepo kwa fluoride kwa kiwango kikubwa sana. Sasa tunatekeleza mradi zaidi ya bilioni 520 katika Jiji la Arusha na baadhi ya vyanzo hivi vya maji vipo katika Jimbo lake. Ninachotaka kumhakikishia bomba kuu lile litakapopita katika maeneo yale ya Mererani na Naisanyi yote yatapatiwa huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kwenda katika Jimbo lake la Simanjiro katika ule mradi wa Olekosmet, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge nipo tayari kuongozana nae katika kuhakikisha tunafika katika mradi ule. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Hali ya ukosefu wa maji iliyopo Simanjiro inafanana kabisa na Mbulu Vijijini, Mheshimiwa Naibu Waziri umefika Mbulu Vijijini. Je, miradi hii ya maji na kisima cha Hyadom ulichotoa ahadi nini unatimiza, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ninachotaka kumhakikishia Mbunge maji hayana mbadala na nilikwishafika katika Jimbo lake na kuna fedha ambayo tuliikuta, nawaagiza sasa DDCA wafike haraka katika kuhakikisha wanakichimba kisima kile ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji ahsante sana.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri na Waziri kwa kazi iliyofanyika na inayotegemewa kufanywa nilikuwa nauliza kwamba katika visima hivyo vimewekwa nguvu ya solar ili kusukuma maji lakini bahati mbaya Hanan’g ni eneo ambalo muda wote halina jua. Je, wanafanya nini ili usambazaji huo uwe unawasaidia wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na swali la pili ni kwamba wakala wa visima ulijaribu kuchimba visima katika kijiji cha Gidamwai au Basodomi pamoja na kijiji cha Gauloli lakini kwa sababu walileta mashine yenye uwezo mdogo wa kuchimba kwenda chini na Hangan’g iko kwenye Bonde la Ufa. Je, ni lini na Wizara iliahidi kwamba ingeleta mashine hizo kuja kuchimba visima hivyo na wananchi walipewa moyo? Naomba nijue ni lini visima vya wakala mashine zawakala wa visima zitakuja Gauloli pamoja na Basodomi ili kuwachimbia hao watu ambao wamepewa moyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge Mama yangu Dkt. Mary Nagu kwa kweli ni mwana mama supavu na amekuwa mpiganaji hasa katika Jimbo lake la Hanang’ na namuomba Mwenyezi Mungu mwanangu siku moja awe kama yeye kutokana na kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikubwa ninachotaka kukisema tumefanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha wananchi wanapata maji lakini kama unavyojua utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na uwepo wa nishati lakini eneo lake kule kumekuwa na hali ya baridi kubwa sana. Sasa kama sisi Wizara ya Maji tutafanya mawasiliano ya karibu kabisa na wenzetu wa Wizara ya Nishati katika kuhakikisha maeneo yale hayana umeme yapelekwe umeme haraka ili wananchi wake waweze kunufaika na huduma hii muhimu sana ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala zima la uchimbaji wa visima hususani kwa wakala wetu wa uchimbaji wa visima DDCA maji ni uhai na sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Hanan’g nimuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya saa saba tukutane ili tufanye mawasiliano ya karibu na wenzetu wa DDCA waende kumchimbia visima vyake ahsante sana.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza wana-Malinyi tunampongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji, mwezi wa Nane alikuja Wilayani akaahidi kutatua matatizo ya maji katika Wilaya ya Malinyi ndani ya miezi miwili na nusu. Mheshimiwa Waziri ahadi hiyo mpaka leo haijatimizwa.

Swali la kwanza, katika Kijiji cha Igawa mradi wa Bonde la Mto Rufiji wamechimba kisima kwa njia ya utafiti, lakini kisima hicho wamekitelekeza. Halmashauri Wilaya ya Malinyi tumeomba zaidi ya mara mbili kibali cha kutumia kisima hiki ili tutengeneze miundombinu kusambaza maji, kutatua kero ya maji kwa wananchi wa Kata ya Gawa. Sasa Serikali inasema nini juu ya kuomba kibali hicho cha kutumia kile kisima walichochimba Rufiji Basin?

Swali la pili, pia Mheshimiwa Waziri aliahidi Tarafa ya Mtimbila; Kata ya Mtimbila yenye vijiji saba ipate maji ya mtiririko. Maji yale hayatoshelezi na kuna mpango pale wa kuboresha ule mradi na Mkandarasi ameteuliwa lakini mpaka leo hajafanya chochote. Vile vile Mheshimiwa Waziri aliahidi kwamba ndani ya miezi miwili na nusu atamwondoa Mkandarasi, atafanya utaratibu wa force account ili mradi ule ukamilike. Nini kauli ya Waziri kwenye ahadi hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji
wake, lakini kikubwa tunatambua maji ni uhai na sisi kama Viongozi wa Wizara ya Maji hatupo tayari kupoteza uhai wa Wana-Malinyi. Kubwa namwomba Mheshimiwa Mbunge kutokana na concern yake na jitihada kubwa ambazo zinafanyika pale kuwasimamia wale Wakandarasi, tukutane leo saa 7.00 ili tuweze kutoa uamuzi wa haraka ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara kwa zaidi ya miaka mitatu imeshindwa kuongeza hata asilimia tatu ya upatikanaji wa maji pamoja na Serikali kuleta pesa nyingi na ipo miradi ya Mayaya na Liyo ambayo kwa zaidi ya miaka mitano haijakamilika:-

Je, Serikali ipo tayari kuunda Tume na kufuatilia kujua kwenye wilaya hiyo kuna tatizo gani ambalo linashinda kutekeleza miradi ya maji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa ambalo nilishukuru sana Bunge lako Tukufu kwa kutupitishia Sheria (Na. 5) ambayo imetupa nafasi sisi kama Wizara ya Maji na rungu la kuwawajibisha Wakandarasi lakini hata kuwawajibisha Wahandisi wetu wa maji. Ninachotaka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tumeshaunda kikosi kazi katika kila mkoa. Labda niagize kikosi kazi hicho kihakikishe kwamba kinafika katika Halmashauri ya Mtwara Vijijini katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji, nami nitafanya ufuatiliaji wa kufika mwenyewe.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniruhusu nami niulize swali la nyongeza katika swali la 79 linalohusu maji. Naishukuru sana Serikali yangu, imetuletea maji kutoka Ziwa Victoria na inachukua kata 10 za Jimbo langu, lakini kuna kata zinazobaki zaidi ya nane hazipati maji:-

Je, Serikali ina mpango gani kupeleka maji kwenye kata ambazo hazipati maji ya mradi wa Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na nimeshafika pale Uyui, lakini ninachotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, Serikali imefanya jitihada kubwa sana zaidi ya shilingi bilioni 600 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi mkubwa utakapofika katika Jimbo lake la Uyui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa naaka nimhakikishie maji yatafika Uyui na maeneo ambayo hayana maji tutahakikisha yale maji yaweze kufika na wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Miradi ya maji mitano iliyojengwa chini ya mpango wa WSDP katika Wilaya ya Karatu, Kijiji cha Buger, Kansay, Getamok bado haifanyi kazi kwa ajili ya kujengwa chini ya kiwango:-

Ni lini Serikali itawawajibisha Wakandarasi hao ili wananchi wapate huduma stahiki?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa ufupi sana, hatuna sababu tena ya kumwona Rais wetu anasononeka au Waheshimiwa Wabunge wanasononeka, mmeshatupa rungu. Ninachotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, baada ya Bunge nitafika Karatu kwa wale wote waliohujumu miradi ya maji, tutawachukulia hatua na kama fedha, watazitapika. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Naibu Waziri alifanya ziara Vilayani Nyang’hwale mwezi wa Nne na kumpeleka kwenye mradi mkubwa wa maji kutoka Nyamtukuza, Kaluma, Bukwimba na kujionea hali halisi ya Wakandarasi wetu wanavyosuasua kuutekeleza mradi huo; na kwa kuwa aliwaita Wakandarasi Wizarani, tulikuja tukakaa nao pamoja; na Mkandarasi anayeitwa Pety, alielezea tatizo la kwamba amecheleweshewa fedha kwa ajili ya kuagizia pump nje:-

Je, Serikali inatoa tamko gani kukamilisha mradi huu kwa haraka iwezekanavyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Nyang’hwale kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Moja ya changamoto kubwa sana ya Sekta yetu ya Maji ilikuwa eneo la maji vijijini. Nilifika Nyang’hwale tukaona Mkandarasi akifanya kazi kwa kusuasua, baadhi ya kazi tulimnyang’anya tukaomba wataalam wetu wa ndani na anaona kasi inavyofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema, tutalifanya hili jambo la haraka. Ile kazi ya kununua pump kama itakuwa imemshinda, tutainunua sisi Serikali ili wananchi wako waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la maji. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara katika mkoa wetu wa Iringa aliweka jiwe la msingi katika mradi mkubwa sana wa maji katika Mji Mdogo wa Ilula:-

Je, ni lini sasa mradi ule utaanza kufanya kazi ili wananchi wa Iringa waweze kutuliwa ndoo kichwani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, anatosha sana mama yangu kwa kuwapigania…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri!

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa ambacho nataka kusema, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, mkandarasi ame-raise certificate kwa ajili ya kumlipa. Tutamlipa kwa wakati.
MHE. RHODA E. KUMCHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Changamoto ya ukosefu wa maji katika Manispaa ya Mpanda pia nayo ni tatizo kubwa. Kata ya Mwamkulu, Kasokola, Kakese pamoja na Makanyagio ni Kata ambazo zina uhaba wa maji na upungufu wa maji. Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari kuhakikisha miradi ya maji pamoja na visima vilivyopo katika maeneo hayo vinatoa maji yenye uhakika ambayo yatawatosheleza wakazi wa Kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Waziri alishafika Mpanda na tumeunda timu maalum kwa ajili ya kutatua tatizo la maji. Kwa hiyo, ipo kazi inayofanyika katika eneo la Mpanda katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini nilikuwa nadhani kuna haja ya Serikali kuwa mfano katika ujenzi wa majengo yake kwa kuweka miundombinu ya uvunaji wa maji kwa mfano kwenye majengo ya hospitali, shule, zahanati na kadhalika. Aidha, nina swali moja la nyongeza. Pamoja na jitihada hizi za kubuni mbinu mbalimbali za uvunaji maji ya mvua, bado kuna uhitaji wa maji katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kigoma, yakiwemo maeneo ya Mwandiga:-

Je, Serikali inatuambia nini au inawaambia nini wananchi wa Mwandiga kuhusiana na upatikanaji wa maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokitaka kuwahakikishia wananchi wa Mwandiga, mimi nimekwishafika pale na Mheshimiwa Waziri amefika, tumetuma fedha kiasi cha shilingi milioni 400. Tumeagiza wataalamu wetu wa ndani wafanye ile kazi. Mpaka sasa uchimbaji wa mabomba wameshachimba, lakini pia mabomba yameshafika pale na tutajenga tenki zaidi ya lita 150,000 katika eneo la Bigabilo katika kuhakikisha wananchi wa Mwandiga wanapata safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mvua kubwa zilizonyesha hivi karibuni Wilaya ya Korogwe zimeathiri kwa kiasi kikubwa miundombinu ya maji na kusababisha shida ya upatikanaji wa maji.

Je, Mheshimiwa Waziri anasema ni upi mkakati maalum na wa dharura wa Serikali kurekebisha miundombinu hii na kurudisha miundombinu hii na kurudisha huduma ya maji kwa wananchi wa Korogwe Vijijini kama wanavyofanya wenzenu kwenye upande wa barabara?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni uhai. Namwomba Mheshimiwa Mbunge tukutane leo saa 7.00 ili tujue namna ya kuweza kuwasaidia wananchi wa Korogwe.
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kama tunavyojua, maji ni uhai na maji safi na salama yanapunguza sana maambukizi ya magonjwa ya matumbo kama vile kipindupindu. Nataka Mheshimiwa Naibu Waziri aniambie:-

Je, ni lini Serikali itajenga visima vya maji safi na salama katika Jimbo la Musoma Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ambacho nachotaka kumhakikishia, pamoja na uchimbaji wa visima, mpaka sasa tumeshasaini mradi mkubwa sana wa Mugango Kyabakari katika kuhakikisha wananchi wa Musoma wanaenda kupata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza. Ahsante sana.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Napenda niseme tu nimefarijika sana kuona kwamba Serikali inatambua kwamba Wilaya ya Chunya ina changamoto ya uhaba wa maji vijijini sababu ya uchache wa vyanzo vya maji. Kwa hiyo, tunapoomba miradi ya Chunya, Serikali iitikie haraka kupeleka miradi hiyo Wilayani Chunya.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivi karibuni alitembelea Wilaya ya Chunya na pale Chunya Mjini alikuta kuna changamoto ya usambazaji wa maji katika Mji wa Chunya. Mheshimiwa Rais aliamuru Wizara itoe fedha ya ziada ili kurekebisha usambazaji wa mabomba ambayo yalikuwa yameharibika na nashukuru Serikali imetoa hiyo fedha na sasa hivi usambazaji unaendelea. Je, usambazaji huu utaisha lini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Mradi wa Maji wa Miji 26 nchini Tanzania, Chunya ni mojawapo ya miji hiyo
26. Je, mkandarasi atakuwa site lini kuweza kurekebisha maji mjini Chunya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza, napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Chunya, Lupa pale, Mheshimiwa Mwambalaswa umekuwa miongoni mwa Wabunge ambao wamekuwa wakifuatilia sana suala la maji katika majimbo yao. Sisi kama Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo na ndiyo maana tumewapa fedha zaidi ya shilingi milioni 372 kwa ajili ya usambazaji wa maji kwa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mbeya katika kuhakikisha wanakamilisha mradi ule. Nachotaka kumhakikishia, kazi kama tulivyopanga itakamilika na tunaiagiza Mamlaka ya Maji ya Mbeya kuhakikisha mradi ule unakamilika kwa wakati ili wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mradi wa Maji kwa Miji 28, kwa kutambua changamoto ya maji maeneo mbalimbali, Mheshimiwa Rais ametupatia fedha zaidi ya dola milioni 500, ni fedha za mkopo, kwa ajili ya miji 28. Mhandisi Mshauri ameshapita site zote, sasa hivi tunasubiri kibali kwa ajili ya kumpata mkandarasi ambaye tutahakikisha tunampata kwa wakati ili aweze kutekeleza miradi hiyo. Nataka nimhakikishie ndani ya mwezi Oktoba mkandarasi atakuwa amekwishapatikana na utekelezaji utakuwa umeanza.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ucheleweshaji wa ukamilishwaji wa miradi ya maji wakati mwingine imepelekea kuwa na matatizo makubwa hasa kwa watumiaji. Hii inaenda sambamba na mamlaka zinazosimamia maji kulazimika kuangalia utaratibu mpya wa kuongeza gharama za maji kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na matokeo yake bill za maji zimekuwa zikipanda sana kila wakati. Hivi tunavyozungumza kuna upandishwaji wa bill ambao unatokana tu na upungufu wa miradi mingi inayoweza ikazalisha maji kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, nini mkakati madhubuti wa Serikali wa kuendelea kuwapunguzia wananchi mzigo wa kulipa bill kubwa kila wakati kutokana na miradi mingi kukwama pengine kutokana na mikataba ya kifedha iliyocheleweshwa ili fedha hiyo iweze kutoka na miradi hii iweze kukamilika kwa wakati?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Stanslaus Mabula, kiukweli ni Mbunge ambaye anayefanya kazi na anawatendea haki wananchi wake wa Nyamagana.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha miradi ya maji inakamilika kwa wakati, sisi Wizara ya Maji tumejipanga baadhi ya miradi mingi tutaitekeleza kutumia Force Account kwa maana ya wataalam wetu kuweza kutekeleza miradi ile ili iweze kukamilika na wananchi wapate huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la bei za maji, tulipata malalamiko kwa wananchi wa Mwanza na Mheshimiwa Waziri ametoa maagizo maalum kwa EWURA kuhakikisha zile bei zinapitiwa ili wananchi wa Mwanza na maeneo mengine waweze kupata bei ambazo zitakuwa rafiki na waweze kupata huduma hii kwa urahisi. Katika kuhakikisha tunaondoa changamoto hii ya bill, sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga na agizo maalumu la Mheshimiwa Waziri ni kuhakikisha kwamba tufunga pre-paid meter katika kuhakikisha wananchi wanalipa kutokana na kile ambacho wamekitumia.

Mheshimiwa Spika, kingine naomba niwasisitize wananchi matumizi ya maji yasiyokuwa na ulazima yanasababisha kuongezeka kwa bili za maji. Leo mvua inanyesha lakini mwananchi anatumia bomba kumwagilia maji maua, haipendezi na wala haifurahishi. Hii ni changamoto lakini naomba Waheshimiwa Wabunge tutoe elimu hii ili kuhakikisha kwamba wananchi wanatumia vizuri maji na wanapata nafuu kabisa katika matumizi haya ya maji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Serikali imekuwa ikitenga fedha kupeleka katika miradi mbalimbali ya maji. Miongoni mwa miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa Mfili ambao uko Wilaya ya Nkasi lakini mradi huo umeshindwa kabisa kumaliza changamoto ya maji. Napenda kujua, Serikali ina mkakati gani wa ziada wa kuweza kumaliza changamoto hizo ili kuendena na kauli ya kumtua mama ndoo kichwani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji vijijini, Bunge lako Tukufu limetenga zaidi ya shilingi bilioni 301. Pia, tumepata zaidi ya dola milioni 500 kwa ajili ya kutatua tatizo la maji zaidi ya miji 28. Vilevile tumepata fedha zaidi ya shilingi bilioni 25.9 kwa ajili ya kukarabati vituo (Payment by Result- PbR) katika kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo tutahakikisha tunafuatilia miradi yetu na mingine tutaifanya kwa kutumia wataalam wetu wa ndani ili kukamilisha kwa wakati na wananchi wapate huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nianze kwa kuipongeza Serikali kwa majibu mazuri ambayo inaonesha jitihada ya kusambaza maji ndani ya Mkoa wa Mwanza. Pamoja na majibu hayo naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

(i) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji alivyokuja Misungwi aliahidi kukamilisha malipo ya mkandarasi mradi huu tajwa hapa wenye gharama ya shilingi bilioni 6.1. Lakini mpaka sasa hivi kwa taarifa niliyonayo ni kwamba kuna sintohamu nyingi, mimi ombi langu moja ningependa kujua ni lini Waziri atapata muda wa kuambatana na mimi pamoja na Mbunge wa Jimbo ili tuende tukae na makandarasi na wananchi ili tupate jibu sahihi ya lini watapata maji safi na salama?

(ii) Mara ya Mwisho Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyotembelea Misungwi aliahidi mradi wa maji wa Misungwi pamoja na Igokelo kukamilishwa na kukabidhiwa mwezi wa tano. Ikasogezwa ikawa ni mwezi wa nane, leo hii tunavyongea ni mwezi wa tisa. Ningependa kujua ni nini mpango wa Serikali wa kukamilisha mradi huu ili wananchi wa Misungwi waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli Mheshimiwa Maria Kangoye ni Mbunge king’anga’nizi katika kutetea wananchi wake. Lakini niungane pamoja na Mheshimiwa Kitwanga kwa kazi kubwa wanaifanya katika Jimbo la Misungwi kubwa ambalo ninachotaka kusema utekelezaji wa mradi wa maji unategemea na fedha nataka nimhakikishie mkandarasi anayetekeleza mradi ule shilingi bilioni 6.1 sisi kama Wizara ya maji hatutakuwa kikwanzo na Mheshimiwa Mbunge na kuhakikishia certificate ile na mradi uweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni kuhusu utekelezaji wa mradi pale Misungwi tuna mradi takribani shilingi bilioni 12 kutokana na kilio cha Mheshimiwa Mbunge Mzee wangu Kitwanga. Wiki ijayo tunakwenda kukabidhi mradi ule ili wananchi waweze kupata maji, na ninataka kumtia moyo Mheshimiwa Kangoye na Mheshimiwa Kitwanga unapotembea na kuzuru wengine naomba usinipite mwokozi, sitowapita nitakuja mwenye Misungwi kushuhudia namna gani wananchi wanaenda kupata maji wiki ijayo. Ahsante sana Mheshimiwa.
MHE. CHARLES M. KITWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya matumaini ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna mradi mwingine ambao umekuwepo kwa muda mrefu sana; mradi wa kutoa maji katika Ziwa Victoria sehemu ya Butimba kupeleka Wilaya ya Ilemela, vilevile kuleta Usagara Wilaya ya Misungwi pamoja na Kisesa Wilaya ya Magu. Kumekuwa na muda mrefu sana tunaambiwa watasaini mkataba. Naomba basi nifahamu leo hii ni lini mkataba utasainiwa na mradi huo uanze haraka iwezekanavyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji napenda kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli Mheshimiwa Kitwanga ni miongoni mwa Wabunge ambao ni wafuatiliaji ususani mambo yanayohusu wananchi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema ukimuona mtu mzima analia ujue kuna jambo. Mheshimiwa Kitwanga sio mara moja analizunguzia hili jambo, nataka nimhakikishie serikali ya awamu ya tano ni serikali ya matokeo sio serikali ya mchakato. Na kwa kuwa sisi tupo karibu sana na Wizara Fedha nikuombe Mheshimiwa Mbunge nikuombe hebu tukutane leo ili tukae na wenzetu wa Wizara ya Fedha hili jambo tuweze kukalisha na wananchi wako waweze kupata huduma hii muhimu sana safi na salama.
MHE. KIZA H. MAYEYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona naomba kuliza swali kama ifuatavyo:-

Halmashauri ya Kigoma Vijiji ina vijiji cha Mwandiga, Kiganza, Bitale, Mkongoro na Msimba ambavyo mpaka sasa wananchi wanateseka kwa kukosa maji, kipundupindu ni cha kwao, lakini kina mama hata ndoa zao zinakwenda kuhatarika.

Ni lini sasa mradi wa Ziwa Tanganyika na ule wa Kigoma Manispaa utafika katika vijiji hivi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza napenda nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba kubwa tunapozungumzia maji, maji ni uhai na sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Mwandiga. Mheshimiwa Mbunge nilivyokuja ziara katika yetu Peter Serukamba alipiga kelele sana kuhusu suala la kupelekewa fedha ili tutekeleze maji na Mheshimiwa Waziri ametuma fedha tayari na ile kazi itatekelezwa na watalaamu wetu wa ndani katika kuhakikisha wana Mwandiga wananufaika na mradi wa uwepo wa Ziwa Tanganyika kati eneo hilo. Ahsante sana.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri yanatia matumaini mazuri. Napenda kufahamu mradi wa maji wa kutoka Bukabile katika Wilaya ya Busega kwenda katika Wilaya za Bariadi Itilima, Meatu na Maswa ni lini mradi huu utaanza kutelezwa, licha kwamba fedha zilishapatikana na mpaka sasa hivi tuliambiwa mwezi wa tisa tutasaini mkataba lakini mpaka sasa hivi hatujasaini mkataba wowote. Nataka kujua ni lini mradi huu sasa utaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge anafanya kazi kubwa sana. Lakini pia napenda nimfahamishe kwamba mkataba tumekwisha kusaini mradi ule na nikuombe Mheshimiwa Mbunge kutokana na kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Waziri ambayo ameitupia jicho katika Mkoa ule wa Simiyu ni kuombe tuweze kukutana tuweze kupeana update lini tutaweza kuutekeleza ili wananchi wako waweze kupata huduma ya maji. Ahsante sana.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Shida iliyopo Mwanza ni sawa na shida iliyopo Mkoani Rukwa, Wilaya Sumbawanga Vijijini Kata ya Kaengesa katika vijiji vya Mkunda, Kaengesa B, Kaengesa A na Italima na vijiji vyote vya wilaya Sumbawanga vijiji.

Ni lini sasa Wizara itapeleka maji katika vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake, lakini kubwa ambacho ninachotaka kusema jukumu la wananchi kupata maji ni jukumu letu sisi Wizara ya Maji na nilishasema si mara moja si mara mbili, sisi ni Wizara maji si Wizara ya ukame tumepata fedha ambazo tumetengewa zaidi ya shilingi bilioni 301 na uwanzaishaji huu wa wakala wa maji vijiji kwa maana ya RUWASA tumejipanga miradi mingi katika kuhakikisha tunaitekeleza kutumia wataalamu wetu wandani, nimhakikishie Mheshimiwa Bupe sisi kama Wizara ya maji vijiji ambavyo ameainisha tunajipanga kuhakikisha tunavitatua ili wananchi wake waweze kupata huduma maji. Ahsante sana.
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza nilitaka kujua mradi wa maji wa Kihonda na Mkundi ambao unaunganisha Mitaa ya Yespa, Kilimanjaro umeshaanza; tunataka kujua ni lini utakamika kwa sababu umechukua muda mrefu mpaka sasa haujakamilika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Mradi wa Maji wa AFD ambao utagharimu Euro milioni 70 Morogoro kama unavyojua kuna kero kubwa za maji; sasa nilitaka kujua ni lini utasainiwa ili uanze kazi uwakombe wananchi wa Morogoro Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji nimpongeze Mheshimiwa Abood ni miongoni mwa Wabunge ambao wachapakazi na amekuwa ni mfuatiliaji mkubwa sana hususan changamoto zinazohusina na wananchi wake, lakini kubwa ambacho ninachotaka kusema pamoja na changamoto zipo jitihada ambazo sisi kama Serikali tunazozifanya katika Mkoa ule kwa maana ya Morogoro Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa Kilimanyari Yespa mradi takribani milioni 715 ambazo tunatekeleza nimwagize Meneja kwa maana Mkurugenzi wa MORUWASA kuhakikisha mradi ule unakamilika kwa mujibu wa mkataba ili wananchi wale waweze kupata huduma ya maji. Na mimi nataka nimhakikishie Mheshimiwa Abood baada ya Bunge nitafika eneo lile kujionea utekelezaji wa mradi ule. Lakini kikubwa kuhusu la huu mradi huu mkubwa kwa maana kuondoa tatizo la maji Morogoro wa Euro milioni 70 ninachotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge ukiona giza linatanda ujue kuna kucha.

Mheshimiwa Abood jana sisi tumefungua tender document kwa maana ya kuwapata wataalam wa ushauri ili kuhakikisha mradi ule unaweza kuanza na wananchi wako wanapata maji. Ahsante sana.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti ninakushukuru, ninaomba niulize swali dogo moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ipo kwenye hatari kubwa la kupoteza fedha takribani shilingi bilioni moja na milioni 600 kutokana na mkandarasi wa Mradi wa Mbuta kuvunja mkataba, lakini vilevile mkandarasi wa Mwakijembe kuamua kusimama kufanya kazi kwa sababu ya uchelewashaji wa fedha.

Ni lini Serikali itachukua hatua za haraka kuhakikisha inaokoa fedha hizi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Dastan Kitandula kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika jimbo lake pale Mkinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti sisi kama Wizara ya Maji tulishasema kwamba hatukuwa na kisingizio chochote, kwamba sasa hivi mmetupa rungu kwa maana uazishwaji wa RUWASA kwa maana Wakala wa Maji Vijijini na tumejipanga vizuri kwa maana agizo la Mheshimiwa Waziri kwa maana baadhi ya miradi ya tutaifanya kwa kutumia wataalamu wetu wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kumhakikishi katika Mkandarasi yule aliyeondoka site hatuna nafasi tena ya kubembelezana ile kazi tutaifanya kupitia wakala wetu wa maji kwa maana ya Uchimbaji wa Maji Visima (DDCA) nawaagiza waende kuifanya kazi ile mara moja ili wananchi waweze kupata maji. Lakini kuhusu mkandarasi ambaye ametekeleza mradi hajalipwa certificate, nataka nimhakikishie ndani ya mwezi huu wa tisa tutamuweka katika orodha ili kuhakikisha kwamba tunamlipa ili wananchi waendelee kutekelezewa mradi wa maji, ahsante sana.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana katika Manispaa ya Mtwara Mikindani yaani Jimbo la Mtwara Mjini kumekuwa na tatizo kubwa la maji kutoka yenye tope jingi kwa muda mrefu na maji hayo yanapita katika mita za wananchi kuwasababishia kulipa bili wakati maji wanayoyapata ni machafu. Pamoja na mambo mengine chanzo kikubwa ni kukosekana kwa chujio katika chanzo cha maji cha Mtawanya.

Swali langu, ni lini Serikali itanunua chujio kubwa la uhakika kwa ajili ya kuchuja maji katika chanzo cha Mtawanya ili kusudi wananchi wanaoishi Mtwara Mikindani wapate maji safi na salama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji niseme kwa ufupi sana ni wajibu na ni haki ya mwananchi kupatiwa maji, si maji tu kwa maana yamaji safi na salama na yenye ubora. Nimefika Mtwara lakini moja ya changamoto kubwa pale ni chujio na nitumie nafasi hii kumwagiza Katibu Mkuu wa Wizara yetu ya Maji kuhakikisha mchakato ule unakamika haraka kwa ajili ya ujenzi wa chujio na wananchi wa Mtwara waweze kupata maji safi salama na yenye ubora. Ahsante sana.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupatikana Mkandarasi wa Mradi wa Lwakajunju katika Jimbo la Karagwe lakini bado wananchi wa Karagwe hawajajua ni lini mkandarasi huyo atakwenda kuanza. Je, ni lini utekelezaji wa Mkandarasi wa maji wa Lwakajunju utaanza ili kuwatua ndoo wakina mama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa jasiri, mpambanaji kwa wanawake wenzake kwa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ninachotaka kusema sisi kama Wizara ya Maji na kupitia Mheshimiwa Rais tunamshukuru sana tumepata fedha zaidi ya dola milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa miradi katika miji 28 lakini tunashukuru jitihada kubwa ambazo zimefanyw ana Waziri wetu kwa maana ya Mheshimiwa Mbarawa kuhakikisha Mhandisi Mshauri amepatikana kwa haraka na ameshapita katika miji yote sasa hivi tunakamilisha document kwa maana ya kupata kibali ili kumpata mkandarasi na ujenzi wa mradi ule uweze kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na kaka yangu Bashungwa siis Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuhakikisha mkandarasi anapatikana kwa wakati na utekelezaji wa mradi wa maji kwa maana ya kumtua mwanamama ndoo kichwani unaanza mara moja. Ahsante sana.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na napenda kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Waziri ulitembelea Jimbo la Mbagala kwenye mradi wa Mgembaki pamoja na Kiwika na ulitoa maagizo kwa sababu miradi hiyo inaendeshwa kiufanisi, wananchi ambao walichangia miradi ile pamoja na Wizara pamoja na watu wa DAWASA wakae pamoja ili waangalie jinsi ya kuiendesha kwa ufanisi, lakini cha ajabu watu wa DAWASA wameingia kule na wanataka kuchukua vyanzo vile bila kushirikisha Kamati zile za wananchi na kuacha kabisa maagizo uliyoyatoa.

Je, utakuwa tayari sasa turudi tena kwa wananchi wale na DAWASA ili tuweze kuangalia jinsi gani ya kuendesha miradi ile kwa maridhiano?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, Mheshimiwa Mbunge unafanyakazi kubwa na sisi kama Wizara ya Maji hatuwezi kuwa kikwazo, nipo tayari kuongozana na wewe. Ahsante sana.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Waziri moja ya ziara ambazo umezifanya Jimbo la Nachingwea ni katika Kata ya Mbondo, Kijiji cha Chimbendenga. Sasa hivi ni takribani miezi minane toka uondoke ule mradi mpaka sasa hivi haujakamilika. Naomba kufahamu commitment ya Wizara juu ya kukamilisha mradi wa maji Chimbendenga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kiukweli nimefika Nachingwea nimejionea kazi kubwa ambazo anazozifanya siyo katika maji tu hata katika maeneo mengine, lakini kikubwa ambacho ninachotaka kusema moja ya changamoto kubwa sana katika sekta yetu ya maji kulikuwa na wakandarasi wengi wababaishaji lakini hata hao wanaotekeleza wamekuwa katika kusuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi hatuna nafasi kama Wizara ya Maji kubembeleza watu. Tunawaomba Wakandarasi wafanyekezi kwa wakati na sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo katika kuwalipa fedha zao katika kuhakikisha wanakamilisha miradi ya maji. Ninachotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, tutafanya mawasiliano na wenzetu wa Nachingwea, tukiona mkandarasi anafanyakazi kwa kusuasua tutamnyang’anya kazi tutaifanya kwa wataalam wetu wa ndani ili mradi wetu uweze kukamilika na wananchi wetu waweze kupata huduma ya maji. Ahsante sana.
MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza niishukuru sana Serikali kwa kuanza kutekeleza ahadi yak. Baada ya Waziri kutembelea na kusikia kilio cha wananchi imetenga shilingi milioni 300 na tayari wamepeleka shilingi milioni 20 na wataalam wameanza kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Katika lot ya miradi ya Kiduduye, Nyagwijima na Muhange, kwa kuwa tayari mradi wa Muhange unatekelezwa: Je, ni lini sasa Serikali itapeleka wataalam na fedha kwa ajili ya miradi miwili ya Nyagwijima na Kiduduye kuanza kutekelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wakati Mheshimiwa Waziri wa Maji akihitimisha hotuba yake ya Bajeti ya mwaka huu, alituhamasisha Wabunge wote kupeleka orodha ya visima vinavyofaa kuchimbwa katika Majimbo yetu, nami nilikuwa wa kwanza kumkabidhi orodha ya visima 15 vilivyofanyiwa utafiti: Je sasa, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kuniambia au kuwaambia wananchi wa Buyungu ni lini sasa ligi itapelekwa katika Jimbo la Buyungu kuanza kuchimba visima hivi 15? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kwa muda mfupi tangu amechaguliwa na wananchi wake. Kikubwa amekuwa mfuatiliaji, nasi kama Wizara hatutakuwa kikwazo kum- support kuhakikisha tunatatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto kubwa sana kusuasua kwa miradi ya maji kulikuwa kunatokana na wakandarasi wababishaji. Sisi kama Wizara ya Maji, tumejipanga, sasa hivi tumeanzisha Wakala wa Maji kwa maana ya RUWASA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie, kwa miradi ile ambayo imekuwa ikisuasua, tutaitekeleza kwa kutumia wataalam wetu wa ndani ili kuweza kukamilisha miradi ile kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, miradi hiyo tutaifanya kwa wataalam wetu na tutawa-support kuwapatia fedha ili miradi iweze kukamilika na wananchi wako, waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la ahadi ya visima, ahadi ni deni. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tukutane tufanye mazungumzo na wenzetu wa DDC ili tuwatume waende kuchimba visima kwa wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu ya maji safi na salama.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwanza niipongeze Serikali kwa juhudi ambazo zinaendelea kuwapatia wananchi wa Jimbo la Kyerwa maji na napongeza kwa ajili ya mradi wa Rutunguru, Kaisho na Isingiro ambao mkandarasi alisimamishwa lakini mradi huu umeanza, naipongeza Serikali.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Mheshimiwa Waziri alipofika Kyerwa tulikaa na kukubaliana mradi huu utakapoanza uweze kwenda kwenye Kijiji cha Kagenyi ambacho tumejenga hospitali ya wilaya, lakini kwenye vijiji ambavyo mmevieleza Kijiji cha Kagenyi hakipo. Ninaomba Mheshimiwa Waziri unihakikishie hospitali yetu ya wilaya ambayo iko kwenye Kijiji cha Kagenyi itapelekewa maji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuna mradi unaoendelea kwenye Kata ya Mabera lakini kumekuwepo na ucheleweshwaji wa kulipwa mkandarasi na sasa hivi anadai zaidi ya milioni 150. Mheshimiwa Waziri ni lini mkandarasi huyo atalipwa ili mradi huu uweze kukamilika na wananchi wa Kata ya Mabera waweze kupata maji safi na salama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kiukweli naomba nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge ni miongoni mwa Wabunge ambao ni wachapakazi na ni wapiganaji hususan maendeleo ya wananchi wake. Kikubwa binafsi nimekwenda na Mheshimiwa Waziri amekwenda kuhusu suala la huu utekelezaji wa mradi huu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa nachotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kutokana na jitihada kubwa ambazo amezifanya ujenzi wa hospitali ile kubwa sisi kama Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo, namhakikishia kijiji kile tutakipelekea huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu swali lake la pili tuna mrai ambao tunautekeleza katika Kata ya Mabira, mradi takribani milioni 586, upo asilimia 80 ambao unatekelezwa na mkandarasi ambaye anaitwa Vumwe Company Ltd anadai takribani milioni 137. Nataka nimhakikishie ndani ya mwezi huu tutalipa fedha ile ili mradi ukamilike na wananchi waweze kupata huduma ya maji na mimi nipo tayari kwenda kuufungua kuambatana na Mheshimiwa Mbunge.
MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mradi wa KASHUWASA wa kutoa maji Ziwa Victoria kuleta katika Mji wa Shinyanga na Kahama. Katika mradi ule vijiji vyote vinavyopitia pembezoni mwa bomba hilo vilipaswa kuunganishwa na maji ya Ziwa Victoria. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri alipofanya ziara na Mheshimiwa Makamu wa Rais alituahidi kutupatia pesa katika vijiji vya Bugwandege, Kata ya Ibadakuli, vijiji vya Mwanubi Kata ya Kolandoto, Chibe katika Kijiji cha Mwakalala pamoja na Kijiji cha Ihapa ambapo tank kubwa la Kashuwasa limejengwa pale lakini wananchi wale hawajapatiwa maji.

Swali langu ni kwamba, sasa ni lini zile pesa alizoahidi zitakuja na ili wananchi wale waweze kupatiwa maji kama alivyoahidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Masele kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Kiukweli kama Serikali tunatambua Mkoa wa shinyanga ni moja ya maeneo yalikuwa na changamoto kubwa sana ya maji na Serikali ikawekeza fedha kwa ajili ya kuyatoa maji Ziwa Victoria na kuyapeleka katika Mji wa Shinyanga.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni kweli vipo baadhi ya vijiji ambavyo havina maji na jukumu la kuwapatia maji ni jukumu letu sisi Wizara ya Maji. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge tukutane sasa haraka na wataalam wetu ili tuangalie namna ya kuweza kutekeleza ahadi hiyo ambayo tuliahidi, ahsante sana.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana Serikali kwa kutuletea maji kutoka Ziwa Victoria na kuhakikisha kwamba Kata tano za Nanga, Bukoko, Mwamashiga, Igunga, Mbutu na Itundulu zitapata maji, lakini nipende kuiuliza Serikali, ni lini sasa Serikali itafikisha maji ya Ziwa Victoria kwenye kata zingine zilizobaki?

Swali la pili, shida ya maji kwenye kata ambazo mabwawa au miundombinu yake iliharibika ni kubwa sana na wananchi wanateseka. Naomna kufahamu, Serikali ina- commitment gani juu ya kukarabati miundombinu hii kwa sababu majibu ya Naibu Waziri yanaonekana ni ya jumla. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana, lakini kikubwa sisi kama Serikali kutokana na changamoto hii ya maji, tumeona haja ya kutumia zaidi ya bilioni 600 katika kuhakikisha tutatatuoa tatizo la maji katika Wilaya ya Igunga, Nzega pamoja na Tabora. Lakini ametaka mkakati ni lini tunakwenda kukamilisha? Mradi ule unatakiwa ukamilike mwaka 2020, Mheshimiwa Waziri ametoa agizo pindi itakapofika mwezi huu wa tisa mradi uwe umekamilika na wananchi waweze kupata huduma ya maji na sisi tutalisimamia hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu swali lake la pili, kuhusu suala la fedha za ukarabati. Katika Bunge lako Tukufu, tarehe sita mwezi huu, tuliidhinishiwa zaidi ya bilioni 610 katika kuhakikisha tunatekeleza miradi ya maji, lakini katika Jimbo la Igunga tumetenga zaidi ya bilioni moja. Nimuombe sana na watalamu wetu wa Igunga waone haja sasa hizi fedha ziwe kipaumbele katika kuhakikisha zinatumika katika kukarabati miundombinu hiyo na wananchi waweze kupata huduma muhimu ya maji.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza, wakandarasi wengi wanaofanya shughuli za miradi ya maji kwenye Wilaya ya Tanganyika, Mradi wa Kamjela, Kabungu, Ifukutwa na Mhese, asilimia kubwa hawajalipwa fedha zao. Je, ni lini Serikali itawalipa fedha hizo kwa ajili ya kukamilisha hiyo miradi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, nikubaliane naye kwanza, ni kweli tulikuwa na madeni takribani zaidi ya bilioni 88, lakini kama unavyotambua, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha, umepata fedha hizo zaidi ya bilioni 88 katika kuhakikisha tunawalipa wakandarasi, na hata hivyo pia tumepata bilioni 12.

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie hata wewe katika Jimbo lako la Kongwa wakandarasi wako sasa tumekwishawalipa. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya saa saba tukutane ili tuweze ku-crosscheck ile taarifa na yeye katika wakandarsi wake katika kuhakikisha tunawalipa. Ahsante sana.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, na kama ulivyosema, ni kweli kwamba swali hili ni la muda mrefu. Kwa kuwa wananchi wa Mkinga wanazo taarifa kwamba mtaalam huyu amekwishapatikana tangu mwezi Novemba, na ilikuwa waingie mikataba lakini yakawa yanafanyika majadiliano yaliyokuwa na lengo la kupunguza scope ya kazi kwa vijiji vile 37, jambo ambalo limeleta taharuki. Je, Waziri yuko tayari kutuhakikishia kwamba hayo majadiliano hayatapunguza wigo ambao utawahakikishia wananchi wa Mkinga vijiji vile 37 vyote vipate maji? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa mradi wa Horohoro umepigiwa kelele sana kwa muda mrefu na sasa unakwenda kutimia, kutekelezwa, na mwezi wa sita sio mbali. Je, Waziri yupo tayari mwezi wa sita utakapofika atoe ahadi kwamba ataandamana na mimi kwenda kuweka msingi wa kuanza ujenzi wa mradi ule kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kiukweli nitumia nafasi hii, dhati ya moyo wangu kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana si kuchangia tu Bungeni lakini hata ofisini amekuwa akija mara kwa mara kuhusu suala zima la mradi huo.

Mheshimiwa Spika, sisi kama viongozi wa Wizara tulikwishasema kwamba hatutakuwa kikwazo kwenye utekelezaji wa miradi ya maji. Wakati mwingine tunatumia muda mrefu sana kwa kuwatumia wakandarasi wetu, sisi kama viongozi tumejadiliana tumeona haja sasa kazi zile zifanywe na wataalam wetu wa ndani ili kuhakikisha kwamba hii kazi inafanyika kwa haraka na wananchi wake waweze kupata maji safi na salama katika kuhakikisha kwamba tunamtua mama ndoo kichwani.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa wakandarasi wa Wilaya ya Nyang’wale wamekuwa wakiuchezea ule mradi na kuchukua muda mrefu na fedha ya Serikali kupotena na juzi Mheshimiwa Naibu Waziri umefanya ziara ukajionea mwenyewe. Je, Serikali inawachukulia hatua gani ya haraka hao wakandarasi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nipende kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya ambayo nimejionea mimi kwa macho nilipoenda hapo Nyang’wale, lakini kikubwa tulikuwa tunatabua kabisa na Waheshimiwa Wabunge wamelalamika sana, hususan utekelezaji wa miradi ya maji vijijini, imekuwa na changamoto kubwa sana na ndiyo maana sisi kama Wizara ya Maji tukaleta Muswada wa kuhakikisha kwamba tunakuwa na Wakala wa Maji Viijini.

Mheshimiwa Spika, tunalishukuru Bunge lako Tukufu kwamba limetupitishia haraka na Mheshimiwa Rais ameshatusainia ule Muswada na sasa ni Sheria. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Viongozi wa Wizara ya Maji, hakutokuwa na Mkandarasi ambaye atashindana na sisi, sisi tumejipanga vizuri, mkandarasi yeyote mbabaishaji ama awe mtalaam, kwa maana ya Mhandisi wa Maji, tutamchukulia hatua haraka iwezekanavyo katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma hii muhimu ya maji.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Swali lililoulizwa namba 256 linafanana kabisa na changamoto iliyopo Wilaya ya Ngara katika mradi wa Muhweza, ni miongoni mwa vijiji 10, lakini mradi huu umechukua muda mrefu sana bila kukamilika. Je, ni lini mradi huu utakamilika ili kuwatua ndoo kina mama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, dada yangu Mheshimiwa Oliver amekuwa mpambanaji mahili katika kuhakikisha kuwapigania wananchi wa Kagera ili waweze kupata huduma hii muhimu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini, kutokana na swali lake nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge, nimelipokea na nilifuatilie kwa haraka na tuweze kuongeza nguzu zetu ili mradi huo uweze kukamilika na wananchi waweze kupata huduma hii muhimu.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, swali hili limekuwa likijirudiarudia kama ulivyosema, lakini nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, na najua Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali sikivu, najua itatekeleza hili kwa sababu ni ahadi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu, kwa sababu wakati wa kuhitimisha bajeti ya Wizara ya Maji, ilituomba sisi Waheshimiwa Wabunge kwa sababu miradi hii mikubwa inachukua muda mrefu, ikatuomba tulete orodha ya pampu au visima vilivyoharibika ambavyo havitoi maji na mimi kama Mbunge wa Jimbo la Sumve nimeshafanya hivyo, nimekuletea Mheshimiwa Waziri. Lini sasa miradi hii midogomidogo ya maji itakamilika na kutekelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimimiwa Spika, nipende kwa dhati ya moyo kumpongeza Mheshimiwa mkongwe mahili katika kuhakikisha kwamba anapigania wananchi wake katika Jimbo la Sumve. Lakini pia amekuwa funzo kwa hasa hususan kwa sisi viongozi vijana tumekuwa tukijifunza mambo mengi sana katika ujengaji wake wa hoja na hata katika suala zima la ufuatiliaji wa mambo mbalimbali yanayohusiana na maendeleo ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, nataka nimuhakikishie Mhehsimiwa Mbunge, Mheshimiwa Waziri alishatoa agizo kwa maana ya Waheshimiwa Wabunge waliohitaji vizima ama ukarabati walete orodha ile kwa haraka, miongoni mwa Wabunge walioleta haraka ni Mheshimiwa Ndassa, nataka nikuhakikishie kwa uharaka ulioufanya na sisi kama viongozi wa Wizara tutalifanya kwa jitihada kwa haraka ili tuweze kumchimbia visima katika kupunguza shida ya maji katika Jimbo lake, ahsante.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza, pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali yetu ya chama cha Mapinduzi kujenga mradi mkubwa wa maji na kufikia kiwango cha asilimia 90 wananchi wanapata maji. Pamoja na mipango iliyopo ya kupeleka maji Mji wa Mgumu, Mji wa Rorya na Mji wa Tarime na Mganga Kiabakari Butiama, Mkoa wa Mara bado unazungukwa na ziwa lakini changamoto ya maji ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua Serikali imejipangaje kuhakikisha Mkoa wa Mara katika Vijiji vyote vya Mkoa wetu ambavyo vinazungukwa na ziwa za Victoria vinapelekewa maji, safi na salama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimimiwa Spika, nipende kumpongeza Mheshimiwa Mbunge mama yangu mama Kilagi kwa kazi kubwa anayoifanya kuwapigania wakinamama wa Mara si mara moja na wala si mara mbili na amewekuwa mfuatiliaji mkubwa sana hususani katika suala hili.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara kwa kutambua changamoto hii ya maji tumetenga fedha au tulizopewa na Mheshimiwa takribani dola milioni 500 katika kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji zaidi ya Miji 28 na tumesha saini mkataba. Nataka nimuhakikishie katika Miji ya Mgumu pamoja na Tarime ile kazi inaenda kufanyanyika kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, lakini kingine tunaenda kusaini sasa wa mkaba wa kupeleka maji Mganga Kiabakari Butiana katika kuhakikisha tuna tatua tatizo hili la maji. Kazi hizi tutazifanya kwa haraka pia bajeti yako umetuidhinishia wizara yetu ya Maji zaidi ya bilioni 610 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka nimuhakikishie sisi kama viongozi kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge tutafanya kila linalowezekana katika kuhakikisha tutatatua tatizo la maji katika Mkoa wa Mara. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza. Mradi huu ingawaji Serikali wanajitahidi kuwatafutia maji wananchi wa manispaa ya Morogoro, mradi huu naona unachukua muda mrefu.

Je, una mpango gani wa kuwapatia maji wananchi wa manispaa ya Morogoro wa muda mfupi wakiwa wanasubiria mradi wa muda mrefu? Hasa kwenye kata ambazo hazipati maji kabisa ikiwepo Kora A na Kora B, Mkundi, Amagadu, Rukobe, Kilimanjaro pamoja na mitaa mingine ya Manispaa ya Morogoro.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, mradi wa Furwe, Mikese unahusisha pamoja na vijiji vya Newland pamoja na mtego wa Simba. Mradi huu wa maji tayari unawapatia maji wananchi wa Furwe. Lakini mpaka sasa hivi ninavyoongea wananchi wa Newland pamoja na mtego wa simba hawajapatiwa maji.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia maji wananchi hawa wa Newland pamoja na Mtegowasimba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze kwa kazi kubwa sana anayofanya kwanza kuwatetea wananchi wa Morogoro. Sio mara yake ya kwanza kuuliza maswali yanayohusiana na maji katika Mkoa wa Morogoro. Lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi katika mamalaka yetu ya maji safi na usafi wa mazingira MORUWASA imekuwa ikitenga 20% katika kuhakikisha inawapatia wananchi maji kabla ya mradi huu mkubwa nataka nimuhakikishie zipo kazi zinazoendelea sasa hivi tupo katika upanuzi wa miundombinu ya maji katika maeneo ya Kihonda Kaskazini maeneo ya Kilimanjaro na maeneo ya viwandani.

Mheshimiwa Spika, lakini pia, tuna utekelezaji wa buster pump station katika maeneo ya Mkundi lakini pia tuna ujenzi wa mradi mkubwa pale zaidi ya milioni 496 katika maeneo ya Mundu na Kilala hii yote ni katika jitihada katika kuhakikisha tunapunguza tatizo la maji katika Mkoa wa Morogoro. Lakini kwa kuwa mama yangu, Mheshimiwa Dkt. Ishengoma amekuwa muulizaji mkubwa sana katika suala zima la maji, nimuombe leo tukutane na Katibu Mkuu tuangalie namna gani tunaweza tukasaidia katika maeneo ambayo aliyoorodhesha ili wananchi wake waweze kupata huduma hii ya maji, ahsante sana. (Makofi)
MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru changamoto ya maji katika Jimbo la Rorya haliko tu katika Mji mdogo wa Shirati, lakini kwenye maeneo mengi katika Jimbo Rorya, lakini Jimbo hili lina bahati ya kuwa na vyanzo vikubwa vya maji ambavyo ni Ziwa Victoria na Mto Mara. Kuna Kata tatu ambazo ziko karibu kabisa na Mto Mara, ambao ni Kata ya Kisumwa, Leba na Nyabulongo, ni nini sasa Mpango wa Serikali kuwawezesha wakazi wa Kata hizi kupata maji safi na salama kutoka Mto Mara.?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Shule za mabweni hasa za wasichana zimekuwa na changamoto kubwa sana ya maji na hivyo kuwafanya wasichana kupoteza muda mrefu kutafuta maji na hii imeenda kuwaathiri ufaulu wao, ningependa kuwafahamu ni kwa sasa Serikali haiji na Mpango maalum wa kutatua tatizo la maji kwenye mabweni hasa ya wasichana, kwa sababu wao wana mahitaji maalum kama ilivyokuja na Mkakati wa kutatua tatizo la madawati, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikupongeze kwa swali zuri lakini kwa namna unavyowapigania wananchi, lakini kikubwa ambacho ninachotaka kukisema. Amezungumza suala la Vijiji vya Kisumwa kukosa maji ambavyo viko karibu sana Mto, mimi nataka nimuhakikishie sisi Wizara ya Maji ni jukumu letu katika kuhakikisha tunawapatia huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, kwanza, nipo tayari kwenda kujionea hali halisi, ili tuweze kuangalia ni namna gani wataalamu wetu wanaweza kufanya mradi ili kuweza kuwasaidia wananchi hao waweze kupata huduma hii muhimu. Lakini kuhusu suala zima la Mpango kuwapatia watoto katika maeneo ya shuleni, upo mpango huo na ulikuwa ukitekelezwa na wenzetu wa TAMISEMI, lakini kwa sasa huduma zote za maji zimeletwa katika Wizara yetu ya maji. Nataka nikuhakikishie kama Mpango ulivyokuwepo na sisi tutausimamia katika kuhakikisha tunatekeleza na maeneo hayo ili waweze kupata huduma hii ya maji katika hizo shule, ahsante sana.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza swali mpja la nyongeza. Kwa kuwa Jimbo la Kasulu Vijijini hasa Kata za Kalela, Kwaga, Rusesa, Muzye, Bugaga na Kagerankanda zina shida kubwa sana ya maji.

Je, Naibu Waziri yuko tayari kuongozana na mimi kwenda Jimbo la Kasulu Vijijini kabla ya Mwaka huu wa Fedha kuisha ili tuangalie ukubwa wa tatizo na ajionee na hatimaye tuweze kuwa na mkakati wa kumaliza tatizo hili la maji kama sio kupunguza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Jimbo lake lakini nataka nimhakikishie sisi kama Wizara ya Maji tumeiona hiyo changamoto katika Jimbo lake. Bunge lako tukufu limetuidhinishia zaidi ya milioni 987 katika kuhakikisha tunaenda kutatua tatizo la maji katika Jimbo la Kasulu Vijijini. Na ninataka nimhakikishie kama Naibu Waziri niko tayari kwenda katika Jimbo lake kuangalia namna gani tunaweza tukashirikiana kutatua tatizo la maji. (Makofi)
MHE. PHILIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Songwe ilipokuwa Chunya kabla hatujagawana kulikuwa na mradi mkubwa wa maji kutoka kwenye miradi ya World Bank vijiji 10 kila halmashauri. Kijiji cha Chang’ombe ambacho Mheshimiwa Naibu Waziri ulikuja mwaka juzi mimi na wewe tukaenda ukahutubia na mkutano na ukawaahidi wale wananchi kwamba watapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kulikuwa na tatizo kubwa la mkandarasi aliyekuwa bado kwenye Halmashauri ya Chunya kwamba kulikuwa na ubadhirifu wa fedha kwenye mradi wa Chang’ombe. Sasa mpaka leo hali iko hivyo hivyo na hata mwaka jana nimekuuliza swali ukasema kwamba utalifanyia kazi. Naomba na leo nisisitize kwamba ni lini unakwenda kumwambia mkandarasi akamilishe kazi pale kijiji cha Chang’ombe Songwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge. Kwanza nimpongeze kwa kazi nzuri ambayo nimeiona kwa macho katika Jimbo lake lakini kikubwa sisi kama Wizara ya Maji, jukumu letu ni kuhakikisha Watanzania wanapata huduma hii ya maji na maji ni uhaki na hayana mbadala. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwakweli tulishatoa agizo na kama agizo lazima litekelezeke. Nikuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya saa saba tukutane ili tuweze kuchukua hatua katika kuhakikisha wananchi wako wananufaika na mradi wa maji. (Makofi)
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, Mbozi katika Kijiji cha Harungu Wilaya ya Mbozi tuna mradi mkubwa wa maji ambao karibu milioni 600 ya World Bank na mradi huu una vituo kama 24 ilikuwa iwe na vituo 24 vya kuchotea maji lakini kwa bahati mbaya sana ule mradi wanasema kwamba umekamilika wakati vituo vinavyotoa maji kati ya 24 ni vituo vinne tu.

Je, Mheshimiwa Waziri, nini tamko lako kuhusu mradi huo ambao ni wa fedha nyingi lakini vituo vingi havitoi maji na tenki lile linavuja?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kutupa taarifa. Nimuagize tu Mhandisi wa Mkoa wa Songwe atupatie taarifa kama ulivyosema ili kuhakikisha kwamba tunalichukulia hatua haraka hili jambo. Ahsante sana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anajibu, ameonesha m ikakati iliyopo kwa Butiama, Kiabakari, Mugango na Vijiji 13 vya Musoma Vijijini lakini katika swali la msingi la Mheshimiwa Sokombi aliweza kuonesha adha ya maji Mkoa wa Mara na akataja na Serengeti. Ningependa kujua mkakati uliopo kwa Wilaya ya Serengeti hasa maeneo ya vijijini ambayo kwakweli wananchi wa pale hawana maji kabisa. Ni mkakati gani Serikali mko nao ikiwemo wa kupeleka visima maeneo ya Serengeti Vijijini, sio pale Serengeti Mji. Mkakati gani upo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili mwezi wa tatu wakati Mheshimiwa Naibu Waziri ukijibu swali langu kuhusiana na adha ya maji Tarime kwa muda mfupi wakati tukisubiria mradi unaotoka ziwa Victoria, niliweza kuulizia vile visima 23 ambavyo Serikali ilisema itakuja kuchimba na DDCA alikuwa ameshafanya usanifu wa awali. Ulinihakikishia kwamba sasa tatizo lilikuwa ni hela na ukaagiza DDCA waende. Lakini ninavyoongea sasahivi ni takriban mwezi mmoja na nusu unaenda bado DDCA hawajafika katika Tarime Mji kuhakikisha kwamba wanatuchimbia vile visima 23 wananchi wa maeneo ya pembezoni waweze kupata maji tukisubiria Mradi wa Ziwa Victoria.

Ni lini sasa wataenda? Maana mpaka sasa hivi DDCA hawajaenda. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, dada yangu lakini kikubwa ninachotaka kukisema sisi kama Wizara ya Maji tunatambua changamoto, si Serengeti tu kwa maana ya Mkoa wa Mara na ndiyo maana katika Miji 28 ambayo tumeiorodhesha kwa ajili ya kutatua tatizo la maji tumeipa kipaumbele zaidi ya miji mitatu kwa maana ya Tarime, Mugumu ambayo ipo Serengeti lakini pia Rorya katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nataka nikuhakikishie tumekwishasaini mkataba katika kuhakikisha utekelezaji huu unakwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia yale maeneo ambayo yapo kandokando na Ziwa Victoria hususan Vijijini tunafanyia usanifu ili kuhakikisha vijiji vile ambavyo vipo pembezoni na Ziwa Victoria ili viweze kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la uchimbaji visima katika Jimbo lako la Tarime tulikwishaagiza na tumepewa agizo hilo kuhakikisha kwamba linatekelezeka lakini kuna mabadiliko tu ya kiutendaji katika Wakala wetu wa Maji na wa Uchimbaji Visima DDCA lakini sasa hivi ameshapatikana Mkurugenzi, tunamuagiza kwa mara nyingine aende kuchimba visima vile ili wananchi wale waeze kupata maji. Kuhusu mradi wako wa Salasala pia tumekwishawalipa. Tunamtaka mkandarasi atekeleze m radi ule na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maji imejenga tanki kubwa la maji mjini Bagamoyo lenye takriban uwezo wa lita 6,000,000 lakini kwanza tunaishukuru sana Serikali kwa kutukumbuka kwa jambo hilo adhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo ni kwamba faida ya tanki hili bado haijaweza kupatikana na kata nzima ya Kisutu, Kata ya Nianjema, Kata ya Magomeni na hata Kata ya Dunda zote kata hizi zinaendelea kupata tatizo la uhaba au kukosekana kwa maji safi na salama kwa sababu hakuna mtandao wa mabomba ya kusambazia maji hayo safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, ni lini sasa Serikali kupitia Wizara ya Maji itaweka mtandao wa mabomba ya kusambaza maji katika kata zote hizi Mjini Bagamoyo. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, amekuwa mfuatiliaji katika kuhakikisha anawasemea wananchi wake wa Bagamoyo ili waweze kupata huduma hii muhimu sana ya maji na nataka nimhakikishie sisi kama viongozi wa Wizara hatutakuwa tayari kupoteza uhai wa wana Bagamoyo katika kuhakikisha wanapata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara ya Maji kupitia Mamlaka ya Usafi na Usafi wa Mazingira DAWASA tumeona haja kabisa ya kukabiliana na kutatua tatizo la maji kwa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na mkoa wa Pwani. Lakini tumejenga matenki makubwa sana ya maji ikiwemo Bagamoyo zaidi ya milioni sita yote ni kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji. Lakini hii ni Awamu ya I ya ujenzi wa matenki, Awamu ya II ni suala zima za usambazaji. Tupo katika hatua ya kupata kibali katika kuhakikisha tunaanzisha sasa mtandao huu wa maeneo ambayo hayana maji, yanapatiwa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tunalifanya hili kwa haraka kibali kipatikane ili wananchi wa maeneo ya Kisutu na maeneo mengine waweze kupata maji safi na salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nilifikiri ni mfupi sana kuonekana, nakushukuru sana kwa kuniona. Ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri wa Maji kwamba kuna mradi unaitwa Malama kule Hanang ambao ungesaidia maji Masakta, Lambo na Maskaroda na umetengewa shilingi bilioni 1.2 miaka mitatu iliyopita lakini mpaka leo wale watu hawakunufaika na hizo hela zilizotengewa.

Naomba kujua ni lini kitafanyika ili Masakta, Lambo na Maksaroda waweze kupata maji? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge mama yangu Dkt. Mary Nagu ni mama wa pekee ambaye amekuwa akiwapigania sana wananchi wake katika kuhakikisha wanapata huduma hii muhimu sana ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie kwa kuwa mradi huu umekwishatengewa fedha wa Malama naomba nifanye mawasiliano na Katibu wangu Mkuu ili katika kuhakikisha tuangalie namna gani tunaweza kuuanza ili wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu sana ya maji.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, Bwawa la Igombe katika Manispaa ya Tabora limejaa tope hivyo kusababisha upungufu wa maji katika manispaa hiyo. Aliyekuwa Waziri wa Maji Mheshimiwa Eng. kamwelwe aliahidi kupeleka fedha TOWASA ili kuweza kusaidia kuondoa tope na kufanya kina cha maji kuendelea kuwa kama kilivyokuwa hapo awali. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha hizo ili wananchi wa Tabora tuweze kupata maji kama ilivyokuwa zamani. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri lakini nimtoe hofu, ahadi siku zote ni deni, sisi kama Wizara ya Maji tutatekeleza deni lile katika kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji. Lakini pia ninataka nimfahamishe kwamba sisi kama Serikali tunatekeleza zaidi ya mradi wa bilioni 600 ambao tunatoa maji Ziwa Victoria kupeleka Tabora pamoja na Miji ya Igunga na Nzega yote ni katika kuhakikisha tunasaidia Mji wa Tabora uweze kupata huduma ya maji. Lakini kuhusu suala zima la ahadi ya kupeleka fedha, ahadi iko pale pale tutatekeleza katika kuhakikisha bwawa la Igombe tunatatua tatizo lile.
MHE. FRED A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Wilaya ya Rungwe ni miongoni mwa wilaya ambazo zina maji mengi ya kutosha na vyanzo vingi lakini wananchi wetu hawana maji ya kutosha. Je, ni lini Serikali itakamilisha miradi ambayo imeanzisha ya maji hususan miradi ya Mwakaleli I pamoja na miradi ya masoko na Kandete pamoja na Kata za Rwangwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kiukweli amekuwa mfuatiliaji hata wewe Naibu Spika, masuala ya masoko na maeneo mengine umekuwa mfuatiliaji na kutuulizwa maswali mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara Mheshimiwa Waziri alinituma, nimekwenda lakini pia Waziri mwenyewe amekwenda na tukawa na kikao cha pamoja na Mheshimiwa Mbunge na sasa hivi kuna kazi ambayo inaendelea kule Masoko. Nataka tumhakikishie sisi kama viongozi tutakuwa wafuatiliaji katika kuhakikisha miradi ile inakamilika kwa wakati na wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza niishukuru Wizara ya Maji, Waziri wake, Naibu na Katibu Mkuu wake kufanya juhudi hizo za kupeleka wataalam kwenye Jimbo hilo la Bunda ambalo lina uhaba mkubwa sana wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa maji yamepatikana katika maeneo 10 ambayo ameshayataja hapa awali na kwa kuwa hizi ahadi zimeanza 2016/2017 mpaka leo 2019. Swali langu la kwanza katika eneo hilo ni kwamba Wizara inazo fedha tayari za kutengeneza mradi wa kuchimba Malambo matano kwa mwaka huu au ni ahadi zile zile za mwaka uliopita? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mheshimiwa Rais tarehe 6 Septemba, 2018 alifika kwenye Jimbo langu kwenye Kata ya Nyamuswa na akiwa Nyamuswa alipata kero kubwa sana ya maji kutoka kwa akinamama wa Nyamuswa ambao wanakabiliwa na kero kubwa sana ya maji. Aliagiza Waziri wa Maji tarehe 6 Septemba, 2018 kwamba baada ya wiki moja Waziri afike pale ahakikishe kwamba anakaa na wanakijiji wa pale akinamama na wadau wa maji wote kwenye Kata ya Nyamuswa kuhakikisha kwamba maji yanapatikana. Sasa ni miezi tisa, Waziri hajaenda pale lakini sio mbaya.

Je, Naibu Waziri ambaye uko sasa ambaye ni Waziri wewe sasa hivi, uko tayari kwenda Nyamuswa kushughulika na lile agizo la Rais? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana hususan katika suala la maji katika Jimbo lake la Bunda lakini nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge. Sisi ni Wizara ya Maji, sio Wizara ya Ukame na hii ni Serikali ya Awamu ya Tano ikiahidi inatekeleza na ikishindwa kutekeleza basi kuna kuwa na sababu mahsusi kabisa katika utekelezaji wake.

Nataka nimhakikishie na ndiyo maana tumetuma wataalam wetu ili kuhakikisha kwamba zile tathmini zilizofanyika ili tuanze utekelezaji ili wananchi wako waweze kupata huduma ya maji. Tunakuomba Mheshimiwa Mbunge utupe ushirikiano wa dhati ili tuhakikishe kwamba wananchi wako yale mabwawa matano tunakwenda kuchimba, ili wananchi waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu kufanya ziara katika jimbo lake kwa Mheshimiwa Mbunge, niko tayari kabla ya Bunge, ili kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo hilo ambalo limeahidiwa. Ahsante sana.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi, Mheshimiwa Bulaya ana swali la nyongeza, Mheshimiwa Bulaya anasema kwamba mkandarasi anayehusika na mradi huu kwa miaka kumi na moja sasa hajatimiza/hajakamilisha Mradi huu na 2017 Mheshimiwa Waziri Mkuu na 2018 Mheshimiwa Rais walitoa tamko juu ya mkandarasi huyu apate kuwekewa nguvu ili aweze kumaliza mradi huu.

Sasa nini hatma ya Mkandarasi huyu ambaye bado yuko site ili mradi huo uweze kukamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nirudi sasa Mkoa wa Dodoma hata Mkoa wa Dodoma kuna maeneo mengi tuna shida ya maji, hususani katika Jimbo la Kibakwe, watu wa Jimbo la Kibakwe wana shida sana na maji safi na salama. Sasa ni lini Serikali itawaangalia wananchi hao ili kuweza kuimarisha afya zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali zuri, lakini kikubwa tukiri kwamba huu mradi ulitekelezwa umechukua muda mrefu na hii yote inatokana kwa baadhi ya miradi kupewa wakandarasi wababaishaji, lakini sisi kama viongozi wa Wizara tumefatilia mradi ule na tumeongeza nguvu yetu kubwa sana katika kuhakikisha mradi ule unakamilika.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa umeshafikia asilimia 92 na tunaendelea kuongeza nguvu katika kuhakikisha mradi ule unakamilika ili wananchi wa Bunda waweze kupata huduma ya maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu eneo hili la Dodoma la Kibakwe, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji na Umwagiliaji tumeliona hilo, nataka tumuagize Mhandisi wa Maji aone namna sasa ya kufanya mradi haraka ili kuhakikisha wananchi wa Kibakwe wanaweza kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, lakini kikubwa katika kuhakikisha Mji huu wa Dodoma unaondokana na tatizo la maji, tuna ujenzi huu wa Bwawa la Farkwa, na tupo katika hatua ya utafutaji wa fedha tunaamini upatikanaji utakapokuwa umepatikana Mradi ule utatatua kabisa tatizo la maji katika Mji huu wa Dodoma, ahsante sana.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiaw Spika, Jimbo la Singida Kaskazini lina uhaba wa maji kutokana na tatizo la kutumia visima vifupi na visima virefu peke yake, lakini tunavyo vyanzo vya mabwawa, ambayo yangeweza kwa ajili ya mradi mkubwa wa maji.

Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutembelea Bwawa la Ntambuko na kuangalia chanzo hiki na tuanzishe Mradi mkubwa utakaoweza kutoa maji yenye uhakika katika Jimbo la Singida la Kaskazini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya katika Jimbo lake na nataka nimuhakikishie, sisi kama viongozi wa Wizara nipo tayari sasa kuongozana naye katika kuhakikisha tunaangalia namna ya kuweza kusaidia tatizo lake.
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na ninatambua kazi nzuri inayofanywa na Waziri na Naibu Waziri katika Wizara hii. Ninayo maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Swali langu la kwanza, je, kwa kuwa vijiji vya Nairombo, Nanjota, Msanga ni vijiji ambavyo vinapitiwa karibu na bomba kuu la Mradi wa Chiwambo pamoja na Mradi wa Shaurimoyo ikiwa ni pamoja na Kijiji cha Nakachindu. Je, Serikali ipo tayari sasa wananchi hawa ambao wako karibu na bomba kuu waweze kupatiwa maji?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili ni kwamba tunao mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka Mto Ruvuma ambao unakaribia kukamilika wenye thamani ya shilingi bilioni 3.6 na mradi huu wakati ukiandaliwa kijiji cha Chipingu ambacho kipo karibu na mradi kilikuwa hakina umeme wa REA na sasa pale pana umeme wa REA.

Je, Wizara ipo tayari sasa kupeleka umeme kwenye mradi huu ambao ni kilometa mbili ili wananchi waweze kupata maji kwa urahisi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo lake lakini kwa kuwa mfatiliaji wa mara kwa mara Wizarani katika kuhakikisha suala la maji linatatuka katika Jimbo lake.

Mheshimiwa Spika, sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo hususan kwa vijiji ambavyo vipo karibu na bomba kuu kupatiwa maji na tumefanya mageuzi makubwa sana katika Wizara yetu ya Maji. Moja ya mageuzi hayo ni kuhakikisha kwamba vijiji vyote ambavyo vinapitiwa na bomba kuu kilometa 12 katika upande wote wa bomba kuu vinapatiwa maji.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama viongozi wa Wizara hatutokuwa kikwazo katika kuhakikisha vijiji vile ambavyo vipo karibu na bomba kuu vipatiwe maji. Lakini kuhusu suala zima la mradi ule wa maji kupatiwa umeme wa REA nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutafanya mawasiliano na Mhandisi wa Maji atuletee document na sisi kama viongozi wa Wizara ili tuweze kuwezesha mradi ule uweze kutekelezeka wa REA, ahsante sana.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza niishukuru Serikali kwa mradi wa vijiji 56 unaoendelea kule Kyerwa usanifu umekamilika. Sasa swali kuna kata ambazo zina hali ngumu sana kama Kata ya Bugomola, Kata ya Kibale, Kata ya Businde na Kata ya Bugala.

Je, Serikali wakati tunaendelea kusubiria huu mradi uanze wako tayari kuwachimbia wananchi visima ili waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru lakini nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri anayoifanya nataka nimuhakikishie sisi tupo tayari na tunalishukuru Bunge lako tukufu limetuidhinishia sisi Wizara ya Maji zaidi ya shilingi bilioni 610 katika kuhakikisha tunatekeleza miradi ya maji bila shaka tutampa nafasi hiyo katika kuhakikisha tunamsaidia visima.
MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, kwanza kabisa kwa masikitiko makubwa napenda kupokea majibu yasiyoleta matumaini ya kupata maji kwa wananchi wenzangu wa Jimbo la Igalula.

Mheshimiwa Spika, Waziri ni shahidi, amekuja Jimboni kwangu na Mheshimiwa Makamu wa Rais tulizungumzia kero hii ya maji, alikuja Mheshimiwa Waziri Mkuu na alikuja Mheshimiwa Rais alitoa ahadi kwamba maji ya Ziwa Victoria yatakuja katika Jimbo la Igalula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Waziri amesema Jimbo la Igalula vijiji vyake viko zaidi ya kilometa 30 linapopita bomba la maji, lakini naomba nikwambie linapojengwa tenki kubwa linalopeleka maji Sikonge na Urambo ambapo ni takribani kilometa 100 na zaidi liko kilometa 18 toka Jimboni kwangu. Lakini wananchi wa Jimbo la Igalula hawapati maji ya ziwa Victoria.

Mheshimiwa Waziri ajiweke katika nafasi yangu aone namna gani tabu napata Majimbo yote ya Mkoa wa Tabora yanapata maji ya Ziwa Victoria kasoro Jimbo la Igalula tu. Lakini ndani yake kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais. Je, Wizara itatekeleza lini ahadi hii ya Mheshimiwa Rais? La kwanza. (Makofi)

Lakini la pili amezungumzia miradi ya Tura, Nsololo na Loya ambayo usanifu wake umeshafanyika muda mrefu na documents zimeshafika Wizarani muda mrefu lakini haipo katika financial year 2018/2019 pamoja na shida kubwa ya maji tuliyokuwa nayo katika Jimbo la Igalula. Je, Waziri ananiambia nini na wananchi wa Jimbo la Igalula leo wanasikia wanataka kusikia kauli ya Waziri? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nataka nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, kiukweli sisi kwa Mkoa wa Tabora tumeona ni eneo ambalo limekuwa na changamoto kubwa sana na ndiyo maana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ametupa zaidi ya shilingi bilioni 600 katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji katika Mkoa wa Tabora kuyatoa maji Shinyanga na kuyapeleka katika Mkoa wa Tabora, lakini kupeleka mpaka Kaliua pamoja na Urambo kwa Mama yetu Sitta.

Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge subira yavuta heri. Tumeanza utekelezaji wa awamu ya kwanza na hatuna kikwazo chochote, nataka nimuhakikishie baada ya maji kufika Tabora tutamhakikishia kwamba tunayapeleka katika eneo lile na ahadi ni deni, tutahakikisha tunatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kumtua mwanamama ndoo kichwani.

Lakini kuhusu suala zima la kibali kuhusu suala la utekelezaji ama usanifu wa Loya, Mheshimiwa Mbunge nataka nimhakikishie naomba baada ya saa saba tukutane na wataalam wetu ili hili jambo tulifanye kwa haraka ili wananchi wake waweze kupata huduma hii muhimu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa maji Kirando Mheshimiwa Naibu Waziri anaujua, Waziri anaujua. Je, lini sasa mtampa mkandarasi kazi aanze kupeleka maji katika Kijiji cha Kirando wakati tumeokoa huo mradi shilingi bilioni tatu ilikuwa shilingi bilioni 7.5 tukawabana majizi na wengine waka fukuzwa kazi kwenda usanifu wa pili mradi umefika shilingi bilioni 4.6 lakini mpaka leo hajapewa mtu mwenye uwezo kwenda kumalizia ule Mradi wa Maji Kirando?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kiukweli amefanya kazi kubwa sana na sisi kama viongozi wa Wizara tumefika katika eneo lile la Kirando kiukweli moja ya miradi ambayo imekuwa ikichezewa ilikuwa miradi ya maji vijijini na tunalishukuru Bunge lako tukufu na Mheshimiwa Rais itakapofika tarehe 1 Julai miradi yote ambayo imekuwa ikisimamiwa na Halmashauri inarudi kwetu katika Wizara yetu ya Maji.

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie makandarasi kwa maana ya Kampuni pamoja na Wahandisi wa Maji ambao wametutia hatiani sisi Wizara ya Maji hawana nafasi ya kazi katika Wizara yetu ya Maji. Lakini makampuni yale mengine yote tutayafutia na katika kuhakikisha kwamba hayatofanya kazi yoyote katika Wizara yetu ya Maji, na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya kutatua changamoto ile na kuokoa fedha tunamuagiza mkandarasi kwa maana ya utangazaji wa kazi ili ianze mara moja ili wananchi wake wa Kirando waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Spika, na mimi nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Bwawa la Farkwa walishafanyiwa tathmini wananchi wa Mwambose na Bubutole na sasa hivi hawaruhusiwi kuendeleza makazi yao wala kuzika watu wanaofariki wanakwenda kuwazika porini.

Naomba kauli ya Serikali ujenzi wa bwawa hili upo? Kama haupo wawaambie wananchi wale ili waweze kuendeleza makazi yao.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji mkubwa sana katika kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma ya maji na maslahi yao mengine.

Mheshimiwa Spika, tunaona kabisa katika mji huu wa Dodoma kumekuwa na ongezeko kubwa na Serikali imehamia, kuna haja sasa ya kuongeza wazalishaji wa maji. Serikali imeona haja sasa ya kuanzisha hili Bwawa la Farkwa katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji Dodoma pamoja na eneo lake la Chemba.

Mheshimiwa Spika, tumekwishafanya usanifu lakini sasa hivi tupo katika hatua ya utafutaji fedha katika kuhakikisha kwamba tunawalipa wananchi fidia na utekelezaji wa mradi ule. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mradi ule upo na sisi kama Serikali tupo mbioni katika utafutaji wa fedha katika kuhakikisha tunawalipa wananchi fidia na utekelezaji uanze mara moja. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.

Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ningependa pia tuyafanye yafuatayo; kwanza kabisa, chanzo cha maji cha Mbwinji kilitengenzwa maalum kabisa kwa ajili ya kusaidia Wilaya za Masasi kama ambavyo umesema, lakini hivi sasa mimi na wewe tunaongea kwa mfano, Kijiji cha Liputu ambapo bomba linalokwenda Nachingwea likitokea Kijiji cha Nangoo kilometa tano tu mpaka sasa kijiji kile hakina maji na kwamba watu wa MANAWASA maka leo hawajaweza kuweka maji kuwaunganishia wananchi wa pale. Je, kauli yako ni nini kuhusianan na hiki kijiji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwenye mpango mkubwa wa bajeti ya Wizara yako iliyoletwa hapa kwetu umeongelea kuhusu mabwawa yatakayojengwa Mihima, Mpanyani pamoja na Chingulungulu, lakini mimi wakati nashauri Serikali nilijaribu kueleza kwamba ni bora tukafanya utafiti ili kuweza kutumia maji safi na salama yaliyopo kwenye hili bomba kubwa la Mbwinji ili kuweza kuyafikisha Lukuledi.

Sasa ningependa kujua kauli yako. Mko tayari kufanyia kazi wazo langu ili wananchi wa Kata ya Lukuledi wapate maji safi na salama badala ya kutegemea maji ya bwawa ambayo ni gharama kubwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri lakini kikubwa ambacho nataka kusemani, maji ni uhai na maji hayana mbadala na jukumu la kulinda uhai wa Watanzania wa mijini na vijijini tumepewa sisi Wizara ya Maji. Nataka nimhakikishie tumefanya mageuzi makubwa sana ndani ya Wizara yetu ya Maji.

Moja ni kuhakikisha kwamba eneo la kijiji ambacho kinapitiwa na bomba kuu, kilometa 12 upande wa kulia ama kushoto vinahakikishiwa vinapata huduma ya maji. Kwa kuwa vijiji hiki kiko katika kilometa tano tutamuagiza Mkurugenzi wa MANAWASA aangalie afanya tathmini ili tuwaangalie wananchi hawa wa Nangoo nao waweze kupata huduma hii muhimu sana ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la kuhakikisha katika eneo hili la Lukuledi wanapata maji ukiachana na mabwawa, sisi jukumu letu ni kuhakikisha Watanzania wanapata maji na kama kuna njia mbadala ambayo itakuwa haitumii gharama kubwa sisi nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tuko tayari na nipo tayari mimi mwenyewe kwenda kuona hali halisi ili mwisho wa siku tuweze kuchukua hatua. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la maji katika Mkoa wa Njombe bado ni kubwa sana. Maeneo mengi, vijiji vingi havina maji na hata Njombe Mjini bado tatizo la maji ni kubwa, je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuleta maji Njombe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama Wizara tunatambua moja ya maeneo yenye changamoto ni eneo la Njombe, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuona haja kabisa ya kutupatia fedha zaidi ya dola milioni 500 kwa miji 28. Katika miji hiyo, mmojawapo katika Mji wa Njombe.

Nataka nimhakikishie tumekwishaandika mkataba haraka kwa maana ya wahandisi washauri wapo katika maeneo mbalimbali, itakapofika mwezi wa tisa wakandarasi wote watakuwepo site, nataka nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, itakapofika mwezi wa tisa wakandarasi watakuwa site katika utekelezaji wa mradi wa maji katika eneo la Njombe. Ahsante sana.
MHE. HASSAN E. MASALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwakunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo ya maji ambayo yametajwakatika Jimbo la Ndanda na huo mradi wa MANAWASA kwa sababu unahudumia Wilaya ya Nchingwea, naomba kufahamu mkakati wa Wizara wa kuhakikisha upanuzi wa miradi hii ya maji katika vijiji vya Nachingwea hasa vijiji vya Namatula pamoja na Mperuka ambako tayari tulishaanza zoezi la kusogeza maji hayo yanayotokana na chanzo cha mto Mbwinji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumjibu Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Masala kwa kazi kubwa kwanza anayofanya katika Jimbo lake lakini kikubwa sisi tuna chanzo hiki cha uhakika wa maji, limebaki tu suala la usambazaji. Lakini Mheshimiwa Waziri wangu wa Maji alikwishatoa agizo kwa mamlaka hizi za maji kuhakikisha kwamba inatenga asilimia 20 ya fedha zao za mapato ili kuhakikisha kwamba wanafanya upanuzi.

Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara tutalisimamia hilo katika kuhakikisha vijiji vyake alivyovieleza vinapata huduma hii muhimu sana ya maji.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza niipongeze Serikali kwamba huu mradi wa Kilelema na Migongo, mmetupatia fedha na kama ulivyosema mwenyewe ni sawa kabisa tunatekeleza mradi ule pamoja na mradi wa kusambaza maji katika Wilaya ya Buhigwe pale mjini. Maswali yangu ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi vijiji vya Rusaba, Nyaruboza na Kibwigwa kama ulivyosema nilitaka tu kupata commitment yako kwamba mwaka 2021 utahakikisha kwamba vipo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunao mradi wa vijiji 26 wa kati ya Serikali ya Ubelgiji na Tanzania ambao unatekeleza miradi ya vijiji 26 Mkoa wa Kigoma na katika Kata zangu za Mnanila, Mkatanga na Mwayaya, mradi ule bado haujaanza pamoja na kwamba tumesaini mkataba wa BTC. Je, ni lini sasa mradi huo utaweza kufanikiwa ili na maji pale yaweze kutoka kwenye vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Albert Obama kwa kazi kubwa anayoifanya pale Buhigwe lakini kikubwa ambacho nataka nimhakikishie kuhusu eneo lake lile la Rusaba, sisi ni Wizara ya maji, nasisitiza tena na si Wizara ya ukame!

Nataka nimhakikishie akapofika mwaka 2020 wananchi wake wa Rusaba tutahakikisha wanapata huduma hii ya maji. Maji ni uhai na sisi kama Wizara ya Maji hatupo tayari kupoteza uhai wa Wana Buhigwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la mradi huu wa Ubelgiji, tupo katika hatua za mwisho za ukamilishaji wa taratibu. Nataka nimhakikishie taratibu zitakavyokuwa zimekamilika mradi ule tutauanza na wannachi wake wataweza kupata huduma ya maji.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana mwezi Septemba Naibu Waziri alifika Monduli na mwaka huu mapema Mheshimiwa Rais alivyokuja Arusha ilizungumzwa habari ya tatizo la maji Monduli na baadae nikaenda Wizara tukakutana na Waziri, Katibu Mkuu na Wakurugenzi wote wa maji. Tukapata kibali cha miradi miwili, Mradi wa Meserani na Mradi wa Nanja na wakaniahidi kwamba mwezi wa nne mradi ule ungesainiwa, mpaka leo mradi ule bado.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua commitment ya Serikali. Ni lini mkataba huu utasainiwa ambavyo Serikali imeshaahidi kwa wananchi wa Monduli?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, anafanya kazi nzuri pale Monduli na mimi nikiri kabisa nilifika pale na moja ya maeneo ambayo alikuwa ameyazungumza na akasema Tenzi za Rohoni, tusimpite, sisi hatukumpita ndiyo maana tukatoa kibali kama Wizara katika kuhakikisha kwamba mradi ule unaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi kama viongozi wa Wizara tulishasema hatutakuwa kikwazo kwenye utekelezaji wa miradi ya maji na ndiyo maana tumetoa kibali. Nimuombe tu sana Mhandisi wa Maji wa Monduli ajitathmini kama sisi Wizara tumekwishatoa kibali yeye anakwamishaje katika utekelezaji wa miradi ya maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya hapa nitafanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha mradi ule unaanza na wananchi wake wanaanza kupata huduma ile ya maji.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Katika Jimbo la Mlimba, Mkandarasi Ben Investment Company Limited anayejenga Mradi wa Maji Chita amesimama kujenga kwa sababu hajalipwa fedha zake kiasi cha shilingi 192,000,000 yapata kama miezi nane sasa. Je, ni lini Serikali itamlipa huyu mkandarasi ili aendelee kujenga huo mradi wa Chita?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge mama yangu Susan Kiwanga, lakini kikubwa ambacho nataka kusema utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha na tunashukuru Serikai kila mwisho wa mwezi huwa wanatoa fedha zile za Mfuko wa Maji zaidi ya shilingi bilioni 12. Nataka nimhakikishie dada mwezi huu tutakapopata ile fedha ya mfuko tutahakikisha kwamba tunakupa kipaumbele ili Mradi wa Chita uweze kuendelea.
MHE.DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka mitatu maji ya Malama maana yake Masakta, Lambo na Masahroda yalitengewa shilingi bilioni 1.2 lakini mpaka leo unaona kwamba matokeo hayafanani na hizo hela zilizotengewa. Naomba Mheshimiwa Waziri anieleze ni kwa nini na awahakikishie watu wa Malama kwamba maji hayo yatapatikana? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, mama yangu Mama Nagu, kiukweli, ni miongoni mwa wamama ambao wamekuwa wapiganaji wa wakubwa sana katika kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma hii muhimu sana ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nimhakikishie tu kwamba, Mhehsimiwa Mbunge, kwa namna anavyozungumza, tukutane basi ili tuangalie ni namna gani ambavyo tunaweza tukalifanya jambo la haraka, ili jambo hili liweze kufanikiwa. Ahsante sana.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la maji kwenye Wilaya ya Rufiji ni kubwa sana hali iliyopelekea nguvu kazi kubwa ya vijana na akina mama kupotea wakijaribu kutembea umbali mrefu, pia wakidiriki kuchota maji kwenye maeneo ya Mto Rufiji na kupelekea wananchi wengi kuchukuliwa na Mamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango gani wa kuja kufanya tathmini ikizingatiwa kwamba Rufiji ni kanda maalum, pia Rufiji tunatekeleza mradi wa uzalishaji wa umeme wa Stiegler’s Gorge. Je, ni lini Serikali itakuja kufanya tathmini halisi kabisa ya tatizo la maji Wilaya yetu ya Rufiji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tatizo la maji kwenye Kata ya Mbwala ambayo Mheshimiwa Waziri amejibia ni kubwa sana tofauti kabisa na majibu ambayo wenzetu wa Halmashauri walimwandalia. Eneo kubwa la Kata ya Mbwala wananchi wanalazamika kusafiri umbali wa kilometa saba mpaka 10 kufuata maji katika maeneo ya Kikobo na maeneo mengine.

Je, ni lini Serikali itadhamiria kabisa kuchimba visima virefu karibu na kwa wananchi hali ambayo hivi sasa imepelekea vijiji vingi wananchi kuhama kutafuta maji kwa sababu wanadiriki kusafiri umbali mpaka wa kiklometa 7 - 10?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Nataka niwahakikishie Wandengereko wote, wamechagua jembe wembe na anafanya kazi kubwa sana katika Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa anataka kujua jitihada za Serikali. Tunatambua kwamba maji ni uhai na ni moja ya changamoto kubwa, lakini sisi kama Wizara ya Maji tumefanya jitihada kubwa ya uchimbaji visima 13 pale yenye thamani zaidi ya shilingi milioni 400, tumeshachimba visima 10. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya ukamilikishaji ule wa visima tutafanya usanifu katika kuhakikisha tunatekeleza miradi mikubwa ili wananchi wako waweze kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka nikuhakikishie kutokana na Kata hiyo ya Mbwala, mimi kama Naibu Waziri nitapata nafasi ya kuja katika Jimbo lako na nitafika katika Kata ya Mbwala ili tuweze kushauriana na kuangalia namna gani tunaweza tukatatua tatizo la maji katika kata yako. Ahsante sana.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili. La kwanza, pamoja na mradi huu kutoa maji katika Mji wa Makambako, bado haijakamilika ikiwepo pamoja na kujenga tenki la lita laki 5 ambalo lilikuwepo kwenye mradi, huo uzio wa eneo la chanzo cha maji pamoja na kukamilisha ofisi ya mamlaka ambayo ilikuwa ndani ya huo mradi. Je, ni lini sasa vitu vyote vitatu vitakamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa kuwa Serikali imetupatia fedha za mkopo nafuu kutoka India kwa ajili ya miradi ile 28 ikiwepo na Makambako, naishukuru sana Serikali, wataalam walishakuja katika Mji wa Makambako wakatembelea na mradi ule umelenga kuhudumia kata tisa ikiwepo Lyamkena na mwisho mpaka Mlowa. Je, ni lini sasa mradi huo utaanza ili wananchi wa Makambako waweze kunufaika na mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza nimpongeze sana Mbunge, mzee wangu Mheshimiwa Deo Sanga lakini ni Mbunge mfuatiliaji; siyo mara moja au mara mbili amekuwa akija katika ofisi yetu katika kuhakikisha wananchi wake wa Makambako wanapata huduma hii muhimu hasa ya maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi ule sasa hivi umefikia asilimia 60 ya utekelezaji, nasi tumekuwa wafuatiliaji wa karibu sana katika kuhakikisha Mji ule wa Makambako unapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie na tumwagize Mkandarasi aongeze nguvu, nasi kama Wizara hatutokuwa kikwazo katika kudai certificate na kumlipa kwa wakati katika kuhakikisha mradi ule haukwami na ukamilike kama ulivyopangwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala zima la utekelezaji wa mradi wa miji 28, nitumie nafasi hii binafsi nimpongeze Mheshimiwa Waziri wangu lakini pia nimpongeze Katibu Mkuu na wataalam wetu kwa jitihada kubwa zilizofanyika katika kuhakikisha mradi huu unaanza mara moja kwa miji zaidi ya 28 Bara na mradi mmoja utakuwa Zanzibar katika kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ninalotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, wataalam washauri walishapita huko katika maeneo. Kikubwa katika mpango wetu ni kuhakikisha kwamba mnapofika mwezi wa Tisa Wakandarasi wawepo katika maeneo yote kwa ajili ya utekelezaji wa miradi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ndani ya mwezi wa Tisa Wakandarasi watakuwa site na utekelezaji utakuwepo, ila la muhimu tunaomba ushirikiano katika kuhakikisha tunashirikiana ili tuweze kutatua tatizo hilo.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba vijiji vitano mpaka sasa hivi vimeshakamilika kupata maji katika Jimbo la Momba ambapo jumla ya vijiji vilivyopata maji sasa hivi vitakuwa ni saba (7) lakini jimbo hili lina vijiji 82 ina maana kati ya vijiji 82 ni vijiji saba (7) tu ndiyo vyenye maji ya bomba. Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba katika bajeti hii ambayo imetengwa ya shilingi bilioni 1.7 inapelekwa kama ambavyo imetengwa ili kwenda kupunguza tatizo la maji kwenye Jimbo la Momba?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, mwaka 1973 katika Mji wa Tunduma uliazishwa mradi wa maji wa mserereko katika Kata za Mpemba na Katete. Mradi ule sasa hivi umekuwa ukitoa maji kidogo sana kutokana na kutokukarabatiwa kwa muda mrefu. Serikali ina mpango gani kukarabati mradi ule ili uwahudumie wananchi wa kata hizo mbili?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kutumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri. Kikubwa ambacho nataka kusema ni kwamba Ilani ya Chama cha Mapinduzi inatutaka itakapofika 2020 tuwe na 85% ya upatikanaji wa maji vijiji na 95% upatikanaji wa maji mijini.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, sisi kama Wizara ya Maji tukaona chanzo pekee ambacho kinaweza kutatua tatizo la maji katika Mji wa Momba ni kutumia Mto Momba. Sasa hivi tupo kwenye hatua ya usanifu, mradi ule utakapoanza utaweza kuhudumia zaidi ya vijiji 21. Kwa hiyo, tunamhakikishia Mheshimiwa Mbunge tutafanya usanifu ule kwa haraka kwa ajili ya utekelezaji wa mradi mkubwa wa kuchukua maji Mto Momba na kuweza kuhudumia vijiji 21.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mradi wa ukarabati wa mradi wa maji kwa ajili ya kuhudumia Kata ya Mpemba, sisi kama Wizara ya Maji tutaongea na Wahandisi wetu Maji pale Tunduma kuhakikisha wanafanya ukarabati huo ili wananchi waweze kupata huduma hii maji. Maji ni uhai, sisi kama viongozi wa Wizara hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Tunduma.
MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kama lilivyo tatizo la maji katika Jimbo la
Momba kwenye Jiji la Mbeya sasa hivi tatizo la maji tunaweza tukasema ni janga. Bonde lote la Uyole maji ni tatizo, ni kukavu kabisa, wananchi wanyonge wananunua maji mpaka ndoo Sh.500, maisha haya yalivyokuwa magumu. Maeneo ya Mwakibete na Ilomba, kote maji ni tatizo. Tumeshauri ili kutatua tatizo la maji Mbeya tutoe maji Mto Kiwira iwe kama source.

Mheshimiwa Spika, cha ajabu akija Rais au Waziri Mkuu maji Mbeya yanatoka, hayakatiki, wakiondoka maji yanakatika. Tatizo nini hasa ambalo linafanya changamoto hii ya maji katika jiji la Mbeya lisitatulike wakati vyanzo vya maji tunavyo na miundombinu ipo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, napenda kumjibu kaka yangu Mheshimiwa Mbilinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo nataka kusema ni kwamba Jiji la Mbeya sasa hivi limekuwa na ongezeko kubwa sana la watu. Kwa hiyo, mahitaji na uzalishaji wetu umezidiwa kutoka na ongezeko kubwa la watu.

Mheshimiwa Spika, mimi kama Naibu Waziri wa Maji nilifika Mbeya na nimejionea hali halisi na kweli nimefika katika chanzo cha Mto Kiwira tumeona hiki ni chanzo pekee ambacho kinaweza kikatumika na kutatua tatizo la maji la Mbeya. Tumekubaliana sisi kama Wizara kuangalia namna ya kufanya usanifu ili sasa tuweze kutumia chanzo cha Mto Kiwira katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji katika Jiji la Mbeya.

Mheshimiwa Spika, lakini haki ya mwananchi ni kupatiwa huduma ya maji. Niwaagize Wakurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira ya Mbeya kuhakikisha inatoa huduma hii maji, kwa uchache wake, lakini kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma muhimu na bora si mpaka kiongozi aweze kufika. Cha msingi nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara tumejipanga kuhakikisha tunatatua tatizo hili la maji katika Jiji la Mbeya.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Changamoto ya ukosefu wa maji iliyopo Momba inafanana kabisa na changamoto ya ukosefu wa maji iliyopo Manyoni Mashariki.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mradi wa Kintinku - Lusilile utekelezaji wake umekuwa ukisuasua, je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka fedha za kutosha ili kukamilisha mradi huo hasa ikizingatiwa kwamba kukamilika kwa mradi huo kutanufaisha zaidi ya wakazi wa vijiji kumi? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, napenda nijibu swali la dada yangu Mheshimiwa Aisharose, kwanza, ni miongoni mwa Wabunge akina mama wafuatiliaji suala zima la maji katika Mkoa wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikubwa nachotaka kusema utekelezaji miradi ya maji unategemea na fedha. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji tutawaangalia kwa namna ya kipekee katika kuhakikisha wakandarasi wanao-rise certificate ya utekelezaji wa mradi wa pale Manyoni Mshariki tunawalipa kwa wakati na utekelezaji wake uendelee na wananchi waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, pia nataka nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge pamoja na Manyoni kuwa na changamoto ya maji lakini sisi kama serikali na tunamshukuru Mheshimiwa Rais zaidi ya dola milioni 500 tulizozipata kwa ajili ya kutatua tatizo la maji nchi zaidi ya miji 28 Tanzania Bara na mji mmoja Zanzibar, sasa hivi Mkoa wa Singida miji mitatu tunaenda kutatua tatizo la maji. Wahandisi Washauri wameshapatikana, nataka nimhakikishie itakapofika mwezi September wakandarasi watakuwa site katika kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo la maji na sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga vizuri sana.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa miaka mingi wananchi wa Jimbo la Handeni Mjini wamekuwa wakiishi katika dhiki kubwa ya maji. Ni lini Serikali itakamilisha Mradi wa Maji wa Handeni Trunk Main kutoka Mto Ruvu kwenda Handeni?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Napenda kumpongeza Naibu Waziri wangu kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, anayelala na mgonjwa ndiye anayejua mihemo ya mgonjwa. Mimi naishi Tanga, najua moja ya changamoto kubwa ni eneo la Handeni. Serikali imeainisha miji 28 na tumeshapata Dola milioni 500 kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa tuko katika hatua ya manunuzi. Ndani ya mwezi Aprili, Wakandarasi wote watakuwa site kuhakikisha tunajenga miradi mikubwa ya maji. Hii ni katika kutimiza azma ya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ya kumtua mwanamama ndoo kichwani. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria umeshafika Mkoani Tabora. Jimbo la Tabora Mjini ni moja kati ya wanufaika wa mradi huo. Je, ni lini Serikali itaanza usambazaji wa maji katika Jimbo la Tabora Mjini ili wananchi wa maeneo ya pembezoni ambao hawana maji kabisa waweze kunufaika na mradi huu? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Moja ya ahadi kubwa sana kwa wananchi wa Tabora ni kuyatoa maji ya Ziwa Victoria na kuyaleta Tabora. Ni jambo kubwa ambalo amelifanya Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na ahadi hiyo imetimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu ni wa zaidi ya shilingi bilioni 600, nasi kama Wizara mradi huu tumeukamilisha na tume-save zaidi ya shilingi bilioni 25. Fedha zile zilizobaki zote zitatumika kwa ajili ya usambazaji wa maji, wananchi wote ambao hawana maji katika Mkoa wa Tabora wataweza kupata huduma ya maji. Kazi hiyo imekwishaanza na wakandarasi wako site kwa ajili ya uendelezaji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa kuwa Serikali ilikuwa na nia njema sana ya sisi kuhamia Dodoma, na Dodoma sasa imekuwa ni sehemu ambayo ina mrundikano wa watu na maji pia yamekuwa hayatoshelezi. Je, ni lini Serikali itatekeleza ile adhma yake ya kuleta mradi wa Ziwa Victoria mpaka hapa Dodoma ili tuweze kupata maji hapa Dodoma?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru sana. Kubwa ni kwamba tulishafanya kikao mimi pamoja na Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Dodoma na ukiwa kama mwenyekiti. Juzi Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo, na ameenda mbali zaidi ya kusema ukizingua, tutazinguana.

Mheshimiwa Spika, nikiwa kama Waziri wa Maji na timu yangu tumeshajipanga na tumeshafanya stadi tunahangaika kutafuta fedha…
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nianze kwa kusikitika sana kwamba majibu anayoandaliwa Mheshimiwa Naibu Waziri na wataalam mengi ni ya uongo. Anaposema kwamba kule Nyanhomango maji yapo milioni ngapi sijui, ni uongo mtupu.

Mheshimiwa Spika, nataka nikwambie mimi ile Ihelele tunayoisema ndiyo chanzo kikubwa cha maji kinachopeleka maji Tabora, Nzega, Kahama, Shinyanga na maeneo mengine. Sisi hatuna tatizo na maji yanakwenda wapi; sisi shida yetu ni tupate maji kwenye kijiji hicho na maeneo yanayozunguka. Ni chanzo kikubwa lakini leo ni zaidi ya miaka 15 wananchi bado wanahangaika na maji kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, sasa kinachosikitisha ni hao wataalam wetu walioko huko. Mimi nimemaliza ziara juzi pale; hakuna hata tone la maji. Hizo DP anazozisema Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba ma-DP yamewekwa zaidi ya miaka 10 yanakwenda Mbarika halafu hayatoi hata maji. Sasa majibu haya Wanamisungwi wajue tu kama hamtaki kupeleka maji, lakini majibu haya yametolewa miaka 15 iliyopita yanaendelea kutolewa hayohayo, hatuwezi kufurahishana kwa staili hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hawa wataalam wanaoandaa haya majibu kwenda kwa Naibu Waziri, ni majibu ya uongo na wanatakiwa kuchungwa.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru sana na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge lakini nataka nimhakikishie kwamba Serikali inafanya jitihada kubwa sana katika Jimbo lake la Misungwi. Hivi karibuni tulikuwa na Mheshimiwa Rais na tumezindua mradi wa bilioni 12 katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maji hayana mbadala na sehemu kwenye chanzo toshelezi, maelekezo ambayo tumeyatoa sisi kama Wizara ya Maji ni kuhakikisha kwamba kabla hatujapeleka maji maeneo mengine, wananchi wa maeneo husika lazima wapate huduma ya maji.

Kwa hiyo, ninachotaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, nimuombe saa saba tukutane na mimi niko tayari kuongozana naye kufanya ziara ili kwenda kujionea uhalisia na kuweza kutoa msaada katika eneo lile ili wananchi waweze kupata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Nimekuwa nikisimama hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kuulizia Mradi wa Maji Kitinku-Lusilile ambao umechukua muda mrefu sana kukamilika, lakini bila ya mafanikio yoyote. Ningependa kupata commitment ya Serikali, ni lini Mradi wa Maji Kitinku-Lusilile utakamilika? Nakushukuru. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Naibu wangu kwa namna anavyojibu maswali vizuri. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kubwa nimefanya ziara katika Mradi ule wa Kitinku–Lusilile, moja ya changamoto kubwa ilikuwa juu ya deni la mkandarasi, alikuwa akidai kama milioni 700. Wizara tumekwishamlipa milioni 700 zile mkandarasi yule. Mkakati wetu ni kuhakikisha mradi ule unakamilika kwa wakati na wananchi wale wanapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wewe utakuwa shahidi hiki ni kipindi changu cha tatu katika Bunge lako Tukufu na siku zote tatizo kubwa kwenye Wizara ya Maji imekuwa ni vitu viwili, mosi; miradi kutokukamilika kwa wakati au ikikamilika haitoi maji. Hii WIzara tangu 2016 imekuwa ikitengewa pesa nyingi, lakini ufanisi na ubora na kile kinachokusudiwa, wananchi wapate maji safi na salama hakipo. Swali langu, je, Serikali ipo tayari kufanya ukaguzi maalum nini chanzo cha miradi kukamilika lakini maji hayatoki au ni nini kinachosababisha miradi ichukue muda mrefu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikushukuru. Nikiri, moja ya changamoto kubwa sana ya miradi yetu ya maji ilikuwa moja, usimamizi lakini Bunge lako Tukufu limeona hili na ndiyo maana tukaanzisha Wakala wa Maji Vijijini kwa maana ya RUWASA, lakini kuhakikisha wahandisi wote wa maji waliokuwa chini ya halmashauri kuja chini ya Wizara yetu ya Maji. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tumeshaainisha miradi zaidi ya 177 na RUWASA imeshaanza kuitatua miradi hiyo zaidi ya 85. Kubwa ambalo nataka niwaelekeze Wahandisi wa Maji pamoja na Wakandarasi, vipo vya kuchezea. Ukishiba, chezea kidevu chako au kitambi, si miradi ya maji, tutashughulikiana ipasavyo! Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kiu ya wananchi wa Makambko inafanana kabisa na kiu ya wananchi wa Same. Mradi umechukua muda mrefu na wakati wa kampeni alipopita Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wakati huo akiwa Naibu Waziri na sasa Waziri ndugu yetu Aweso, aje mara moja na yeye akasema yale yale maneno ya kutokushika kidevu lakini uchezee kitambi. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, je, ni lini wananchi hao wa Same watasambaziwa maji?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana mama yangu Shally Raymond, amekuwa mpiganaji mkubwa sana hususan wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro; Moshi, Same na Mwanga waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, moja ya miradi ambayo ilikuwa imechezewa na wakandarasi wababaishaji ni Mradi wa Same – Mwanga na nilipata nafasi ya kwenda katika mradi ule, tumekwishawaondoa wakandarasi wale. Kubwa kazi hii tumeweza kuwapa wenzetu wa DAWASA kuona tunaweza kuifanya kwa force account, mwisho jana Katibu Mkuu alikuwepo huko, tumewekeza nguvu zetu kuhakikisha mpaka Desemba mradi ule uwe umekamilika na wananchi wale waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kuuliza swali moja la nyongeza kwa niaba ya wananchi wa Sengerema. Ni kwamba tuna miradi mikubwa, Mradi wa Sengerema ni mradi mkubwa katika nchi hii, una bilioni 23, lakini una deni la shilingi milioni 300 kutoka TANESCO. TANESCO wamekuwa wakikata maji toka mradi huu umefunguliwa na kuna mabomba yako Sengerema pale yanasubiri kusambazwa kwenye hiyo miradi ya maji.

Je, Waziri yuko tayari kukubali wananchi wa Sengerema wauze yale mabomba halafu wakalipie umeme ili tukae salama sisi.

Mheshimiwa Spika, hili jambo ni kubwa na namwomba Mheshimiwa Waziri wa Maji, yuko tayari kufuatana na mimi kwenda Sengerema akaone hii hali?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza ukimuona mtu mzima analia ujue kuna jambo. Sasa niko tayari kuongozana naye lakini hapa niwe muwazi, Serikali eneo la Sengerema imewekeza zaidi ya bilioni 20, imetimiza wajibu wake, lakini ni haki ya mwananchi kupatiwa maji nay eye ana wajibu wa kulipia bills za maji. Kwa hiyo kubwa yawezekana kuna changamoto pia ya kiutendaji kushindwa kusimamia na kukusanya mapato. Haiwezekani uwe na mradi wa bilioni 20, halafu ushindwe kukusanya mapato angalau kulipia umeme, haiwezekani! Kwa hiyo nitafika na tutaangalia namna gani ya kumsaidia. Tukiona mtendaji yule anashindwa kutimiza wajibu wake, tutashughulikiana ipasavyo kuhakikisha wananchi wa Sengerema wanaendelea kupata huduma ya maji. (Makofi)
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza kwenye sekta hii muhimu. Suala zima la maji ya Mradi wa India imekuwa ni changamoto kubwa sana katika hii miji 28 na ambayo inasababisha Watanzania wengi kukosa maji. Nataka tu kujua, Mji wa Chemba ambao umekuwa kwenye ahadi ya Miradi ya India miaka nenda miaka rudi, ni lini Serikali itapeleka mradi mbadala wakati Watanzania wanaendelea kusubiri huo Mradi wa India ambao umeshindwa kutekelezeka kwa kipindi cha muda mrefu?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nimtoe hofu dada yangu Kunti, Mheshimiwa Mbunge. Serikali haijashindwa, Serikali ipo kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji katika Taifa letu na ndiyo maana tuna miradi mikubwa mbalimbali ambayo tunaitekeleza. Katika eneo hili la miji 28, wewe ni mmojawapo ambao sisi umetumia hatua ya kutuita kuona hatua ya utekelezaji wake. Nataka nimhakikishie ukiona giza linatanda ujue kunakucha, timu yetu ya evaluation imekamilisha kazi. Naomba watupe nafasi waone namna gani Serikali hii ya mama yetu Samia Suluhu ambaye ametupa maelekezo mahsusi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunawatua akinamama ndoo za maji kichwani itafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Chemba pamoja na hiyo miradi mikubwa ambayo ipo kimkakati, Mheshimiwa Mbunge tumekwishakutana nae ametuomba visima vya dharura katika eneo lake la Chemba ili wananchi wake waweze kuapat huduma ya maji. Ahsante sana.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, natumia nafasi hii kumshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa huu mradi umechukua muda mrefu sana, zaidi ya miaka kumi, kukamilika, na kwa kuwa Waziri ameahidi kwamba ndani ya huu mwaka mmoja huu mradi unakuja kukamilika; ninapenda kujua sasa Wizara inakuja na mikakati gani ndani ya huu mwaka mmoja kuhakikisha maji yanafika katika vijiji 11.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa huu mradi vilevile unanufaisha kata tatu ambazo zina miradi mikubwa ya kimkakati ukiwepo mradi wa ujenzi wa reli lakini vilevile na kituo cha afya. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa haraka kupeleka maji katika Kata ya Kintinku na Maweni?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Naibu Waziri wangu kwa kazi kubwa na nzuri namna anavyojibu maswali yake, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilifanya ziara katika Mradi wa Kintiku-Lusilile, ni mradi ambao umechukua muda mrefu sana na mkandarasi alikuwa akidai kiasi cha pesa. Tumeweza kumlipa kiasi cha shilingi milioni 500, lakini pia tumepokea fedha shilingi bilioni 25, kwa ajili ya kuwalipa wakandarasi. Nataka nimhakikishie mmoja wa wakandarasi ambao watalipwa fedha ni Mradi huu wa Kintiku-Lusilile. Kwa hiyo maelekezo ya Wizara na wakandarasi wote watakaopata fedha ni kuhakikisha wanakamilisha miradi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako nataka niliambie Bunge lako Tukufu jana Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo mahususi katika Wizara yetu ya Maji, na sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji tumeyapokea na tutayafanyia kazi kikamilifu. Lakini naomba nitume salamu kwa wahandisi wa maji pamoja na wakandarasi; wakae mguu sawa, na sisi tutafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii. Kwa kuwa, tatizo la maji katika Jimbo la Serengeti ni sawa kabisa na tatizo la maji kule Namtumbo. Naipongeza sana Wizara, rafiki yangu Mheshimiwa Jumaa amejitahidi sana kuhakikisha mradi wetu wa maji hasa ule wa chujio unakamilika hata hivyo mpaka sasa hivi mradi ule bado haujakamilika, lakini pia kupeleka maji katika vijiji vya Jirani. Je, ni lini Serikali itakamilisha miradi yote hii miwili?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri wangu kwa namna bora na nzuri ya kujibu maswali. Kweli nimeamini mtoto wa samaki hafundishwi kuogelea, hongera sana Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa ambalo nataka niliseme ni kwamba Wizara ya Maji tumepokea miradi 177 ambayo ni kichefuchefu na ilikuwa ikichafua Wizara. Mkakati wa Wizara baada ya kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA), tukasema miradi hii yote kichefuchefu ikiwemo mradi wa Mugumu ambao ulikuwa ukichafua, sasa hivi tunaukwamua. Katika wiki hii tunatoa fedha zaidi ya milioni 300 kuhakikisha tunakamilisha mradi ule na wananchi wa Mugumu waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Ndani ya Mkutano huu wa Tatu Serikali ilikuja hapa ikatoa majibu kwamba mradi huu wa HTM utaanza mwezi wa Aprili. Wananchi wamekuwa wakiniuliza mara kwa mara mwezi Aprili umepita na mradi haujaanza. Sasa kwenye majibu ya Serikali wanadai kwamba mradi utaanza kabla ya mwaka huu wa fedha kuisha. Mwaka wa fedha unaisha mwezi mmoja mbele, naomba nijue ni lini hasa mradi huu utaanza kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Handeni? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, wananchi wa Jimbo la Handeni tuna dhiki kubwa ya maji na tumekuwa tukinywa maji kwenye mabwawa kwa miaka mingi lakini mabwawa haya pia yamebebwa na mvua katika misimu iliyopita. Bwawa la Kwimkambala pale Kwendyamba, Kumkole pale Mabanda pamoja na Bwana la Mandela pale Kwenjugo; yote haya yamebebwa na mvua.

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa mabwawa haya ili wananchi angalau tuendelee kunywa maji tukisubiria Mradi huu wa HTM. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru lakini nimpongeze Naibu wangu kwa namna anavyojibu maswali. Kubwa nimpongeze sana kaka yangu Reuben amekuwa amefuatilia mradi huu mkubwa wa miji 28.

Mheshimiwa Spika, kesho nimewaalika Wabunge wote wanaohusiana na mradi huu wa miji 28 tuwape commitment na uelekeo mzima wa mradi huu. Kwa hiyo nimwombe sana kesho katika kikao ambacho tutakachokaa tutatoa commitment ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kubwa tunatambua kabisa kwa eneo la Handeni palitokea mafuriko yale mabawa yalikwenda na maji, Mheshimiwa Mbunge kwa udharura huo na sisi tuna pesa za dharura, naomba saa saba tukutane tuone namna ya kuweza kusaidia wananchi wake waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli sijapata majibu mazuri namna hii katika Serikali hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, namshukuru sana. Nawapongeza sana Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nina maswali madogo tu mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile vijiji vitano alivyovitaja Ikongolo, Kanyenye, Kiwembe, Kongo na Hurumbiti ni bakaa ya mradi wa Ziwa Viktoria na hela zake zipo shilingi bilioni 25. Je, lini mradi huu wa kumalizia vijiji hivyo vitano utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa vile wananchi wangu wa Jimbo la Tabora Kaskazini wanahitaji mafunzo na elimu kuhusu matumizi ya maji hayo, lakini vilevile kuhusu utunzaji wa miundombinu ya maji, je, lini elimu hiyo kwa wananchi itaanza kutolewa? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Mzee wangu Almas Maige kwa kazi kubwa na nzuri hasa ya kuwapigania wananchi wake wa Tabora kuhakikisha maji tunayatoa Ziwa Viktoria na kuyapeleka Tabora, Igunga, Nzega. Historia itakukumbuka mzee wangu, Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake kwamba lini tutatekeleza mradi katika vijiji vitano, nataka nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, sisi Wizara ya Maji si Wizara ya Ukame, vijiji vile vitano vilivyobaki tunakwenda kuvikamilisha mara moja ili wananchi waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa kuhusu suala zima la elimu katika eneo lile la Tabora, Wizara ya Maji tumetekeleza mradi mkubwa sana wa zaidi ya bilioni 600 katika Mji wa Tabora, Igunga, Nzega. Pasipo elimu kwa wananchi inawezekana wakahujumu miundombinu ya maji. Hii ni kazi yetu sote Mheshimiwa Mbunge, mimi Waziri wa Maji na Waheshimiwa Wabunge wote kuhakikisha kwamba tunatoa elimu ya kulinda na kutunza vyanzo na miundombinu ya maji ili kuhakikisha wananchi hawa wanaenda kuvilinda na kuvitunza, ili miradi hiyo iwe na manufaa kwa vizazi vya sasa na vya baadaye. Ahsante sana.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Napenda kuuliza swali langu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na Wizara ya Maji kusambaza maji zinaweza kuwa bure kama gharama za kuunganisha maji hazitashushwa. Swali langu ni hili, kwa nini Serikali isishushe gharama za kuunganisha maji, ikiwa ni pamoja na kuzuia wananchi kulazimishwa kununua vifaa vya kuunganisha maji kwenye Mamlaka za Maji na gharama zake zikawa kama umeme wa REA shilingi 27,000? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Sisi kama Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji, si maji tu, lakini kwa gharama nafuu. Kwa hiyo, nikiwa Waziri wa Maji tumepokea ushauri, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mji wa Munze katika Wilaya ya Kishapu ni mji ambao umepata maji ya Ziwa Viktoria. Kumekuwepo na tatizo kubwa sana la maji kukatika katika Mji wetu wa Kishapu, wa Munze. Je, ni tatizo gani linalosababisha maji haya kukatika huku tukitambua kwamba maji ya Ziwa Viktoria yamekuwepo kwa wingi sana na halipo tatizo la maji, lakini changamoto kubwa ni kukatika kwa haya maji? Naomba majibu.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Kishapu kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tuna mradi ambao tumepeleka maji ya Ziwa Viktoria katika Jimbo lake la Kishapu. Kukatika kwa haya maji changamoto kubwa ilikuwa ni deni la umeme. Sisi kama Wizara ya Maji tumeshatoa milioni 600 kuwapa wenzetu wa KASHWASA kuhakikisha wanalipa deni lile TANESCO ili wananchi waendelee kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Wizara ya Maji ina dhamira njema na wananchi wa Jimbo langu la Manyoni Magharibi. Kuna visima ambavyo vimeahidiwa na Wizara katika Vijiji vya Jeje, Njirii, Kamenyanga, Itagata, Ukimbu, Chabutwa, Makale na Kalangali na Itagata, je, ni lini wataenda kuchimba visima hivi?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Kubwa nimuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya dakika chache nakuja kuwasilisha bajeti yangu ya Wizara ya Maji na bajeti yetu imesikiliza ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tumezingatia maelekezo yako katika kuhakikisha wananchi wako tunawachimbia visima. Ahsante sana.
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na utoaji na usambazwaji wa maji mijini na vijijini bado kuna malalamiko makubwa sana ya ankara za maji kutokuwa na uhalisia. Je, Serikali ina nini la kusema au kuna tamko gani la Serikali ili kuondoa mkanganyiko huu ambapo wananchi wanabambikwa ankara ambazo hazina uhalisia? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mheshimiwa Mbunge lakini niseme tu wazi ni haki ya mwananchi kupatiwa huduma ya maji na mwananchi ana wajibu wa kulipia bili za maji, lakini wajibu huo wa kulipia bili za maji zisiwe bambikizi. Kwa hiyo, maelekezo ya Wizara yetu ya Maji kwa Mamlaka zote za Maji nchini watoe bili halisia ambazo zimeidhinishwa na EWURA. Ikiwa kuna Mkurugenzi au msoma mita kwa makusudi anambakizia mwananchi bili ya maji tutashughulika naye.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa juhudi zinazoendelea za kuwapatia maji wananchi wa Jimbo la Kyerwa kwenye Mradi wa Vijiji 57.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ziko kata ambazo haziko kwenye Mradi wa Vijiji 57, kama Kata ya Bugara, Kibale, Businde pamoja na Mlongo. Nini juhudi za Serikali kuwapatia wananchi hawa maji?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana sana kaka yangu Mheshimiwa Bilakwate kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Jimbo lake la Kyerwa. Kubwa ambalo nataka kusema, sisi kama Wizara ya Maji, tumejipanga na zaidi ya miradi 1,527 tunakwenda kuitekeleza katika maeneo ya vijijini katika kuhakikisha wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishe maeneo ambayo hayana maji, sisi kama Wizara tumejipanga kuhakikisha tunawafikishia hii huduma ya maji safi na salama.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana, sana, sana, ambayo kimsingi yatawatia moyo sana wapiga kura wangu pamoja na wananchi wa Jimbo la Singida Magharibi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Mradi wa Maji wa Kata ya Mtunduru umechukua muda mrefu sana katika kukamilika.

Nilikuwa nataka nijue; je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutoa agizo kwa Serikali ku-release fedha haraka ili mradi wa maji wa Mtunduru pamoja na vijiji vya Igombwe uweze kukamilika haraka?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza kama yangu Mheshimiwa Kingu. Kiukweli wewe ni Mbunge unayetosha mpaka chenji inabaki. Kubwa ambalo ninataka niseme, sisi Wizara ya Maji tunapokea fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji kupitia Mfuko wa Maji kila mwezi. Ndani ya mwezi huu tutatoa fedha kwa ajili ya mradi wako kuhakikisha tunaukamilisha. Ahsante sana (Makofi)
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Kwa kuwa kuna kero kubwa ya maji katika Kata za Ruaha, Mikumi, Ulaya, Tindiga na Malolo; na Serikali inatambua hilo:-

Je, ni lini Serikali itakwenda kutatua shida ya maji katika Kata hizo? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge, lakini sisi kama Wizara ya maji kwa dhati kabisa tunataka kumaliza tatizo la maji Mikumi pamoja na Morogoro. Hakuna sababu hata moja ya wananchi wa Morogoro na Mikumi kulalamikia suala la maji ilhali wana vyanzo vya maji vya kutosha. Kwa hiyo, sisi kama Wizara ya Maji tumejipanga sasa kujenga miundombinu ili wananchi wako wa Mikumi waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upendeleo mkubwa baada ya bajeti nitafika katika Jimbo la Mikumi ili kuhakikisha kwamba tunakwenda kufanya kitu pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Changamoto za maji zilizopo katika Jimbo la Kalenga kwa Kata za Lumuli, Masaka, Kiwele, Luhota, Kalenga yenyewe na Magulilwa zimekuwa ni kubwa sana:-

Je, Serikali mna mkakati gani sasa wa kuhakikisha wananchi hawa wanapata huduma za maji safi na salama? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kilio hiki cha wananchi wake, lakini kubwa sisi kama Wizara ya maji, tumepewa maelekezo mahususi kabisa na Mheshimiwa Rais wetu kipenzi Mama Samia Suluhu Hassan; na akaenda mbali kabisa, kwamba tukizingua atatuzingua. Sisi hatupo tayari kuzinguliwa, tutakwenda kuhakikisha kwamba wananchi wako wanapata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kumwuliza swali Mheshimiwa Waziri kuhusiana na mradi wa maji wa Hanga, Mawa na Msindo ambapo upembuzi yakinifu ulishafanyika na uko Wizarani:-

Je, Serikali inaweza kutueleza ni lini mradi huo au inaweza ikaweka katika bajeti hii mradi huo ukaanza? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeze kaka yangu Mheshimiwa Kawawa kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Jimbo lake la Namtumbo. Wizara yetu ya maji jukumu letu mahsusi ni kuhakikisha wananchi wa Tanzania na Namtumbo wanapata huduma ya maji. Namwomba sana kaka yangu, eneo kama mradi unahitaji kibali na sisi kama Wizara ya Maji tupo tayari kutoa kibali na mradi ule uanze na wananchi wako waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Nami naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kuhusiana na ahadi ya Serikali ya kupeleka matawi ya maji katika vijiji vilivyopo pembezoni mwa bomba kubwa la maji safi na salama yaliyotoka katika mto simba Mlimani Kilimanjaro kwenda Longido na vijiji hivyo ni Eliarai hasa Kitongoji cha Himotong, Tingatinga, Ngareiyani na Sinya?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge. Kiukweli historia kubwa ambayo umeiacha Longido ni juu ya ule mradi wa shilingi bilioni 16 ambao tumeutekeleza katika Jimbo lako.

Kwa hiyo, eneo lile ambalo limepitwa na bomba kuu vijiji upande wa kulia wa bomba kuu na kushoto, zaidi ya kilometa 12 navyo tutavipatia huduma za maji safi na salama. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Liwale ina Kata 20 na vijiji 76, lakini bado upatikanaji wa maji ni wa shida sana hasa hasa kwenye vijiji vya Kihangara, Makata, Kikulyungu, Nahoro, Lilombe, Ngorongopa, Mkutano, Mtawatawa, Kimambi na Nanjegeja.

Mheshimiwa Waziri, ni lini vijiji hivi vinaweza kupatiwa maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ukimwona mtu mzima analia ujue kuna jambo. Mheshimiwa Mbunge wa Liwale amekuwa akilia sana juu ya suala zima la maji katika Jimbo lake. Sisi kama Wizara ya Maji tumewapatia fedha wakala wa Uchimbaji visima DDCA waende katika Jimbo lako la Liwale waende wakachimbe visima ili wananchi wako waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana nami kuniona. Changamoto zilizopo katika Jimbo la Singida Magharibi hasa kwenye miundombinu ya maji zinafanana sana na zile zilizoko Arumeru Mashariki, hususani Kata ya Keri ambayo ina taasisi nyingi za Serikali:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuja kukarabati ile miundombinu na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata maji safi na salama kwenye kata hiyo pamoja na Embaseni, Maji ya Chai, Kikatiti, Maroroni na Majengo? Nakushukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru. Nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwani amekuwa mfuatiliaji mkubwa hususan wananchi wake wa Arumeru. Tunachotaka ni kujenga commitment katika Wizara yetu ya Maji kupitia bajeti yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maoni makubwa ya Waheshimiwa Wabunge tumeyazingatia, nataka nikuhakikishie maeneo ambayo ameyaeleza tutayafanyia kazi kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Serikali iliahidi kupeleka visima 23 kwenye Halmashauri ya Mji wa Tarime kuweza kupeleka visima hivyo pembezoni mwa kata ambazo zipo nje ya mji tangu mwaka 2018.

Ni lini sasa Serikali itakwenda kuchimba visima hivyo wakati tukisubiria mradi wa Ziwa Victoria?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana dada yangu Mheshimiwa Matiko. Maji hayana mbadala. Maji ni uhai, nasi hatupo tayari kupoteza uhai wa wana Tarime. Kabla ya mwaka huu wa bajeti kwisha tutafanya shughuli hiyo kuhakikisha wananchi wake tunawachimbia visima vya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa pamekuwa na malalamiko ya mara kwa mara kwa watumiaji wa maji kubambikizwa bili:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha mfumo wa kufunga mita ambao zitakuwa za malipo kwanza kama Luku ya umeme?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge, Mzee wangu, Mzee Hussein. Kiukweli kongwe huvusha, tunakushukuru sana. Kubwa ambalo nataka kusema, kizuri huigwa. Tumeona wenzetu wa TANESCO za kuwa na mita hizi za Luku, nasi kama Wizara ya Maji tuna pre-paid meter ambapo tumeshaanza na tumefunga katika baadhi ya taasisi. Mkakati wetu na maelekezo kwa mamlaka zetu zote za maji ni kuhakikisha tunajielekeza huko katika pre-paid meter ili kuhakikisha kwamba wananchi wanalipa bili halisia bila ya usumbufu wowote. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kufahamu kwa Mheshimiwa Waziri: Ni lini miradi mikubwa ya kutatua changamoto ya maji kwa hatua ya awali iliyopo Jimbo la Ndanda itatekelezwa, zaidi kwenye Kata za Namajani, Mpanyani, Msikisi pamoja na Chiwale? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nampongeza Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Cecil Mwambe, kwa kweli amekuwa mfuatiliaji mkubwa hasa katika Jimbo lake la Ndanda. Ahadi ambayo nampa katika maeneo ya kipaumbele nitakayokwenda mimi mwenyewe baada ya Bajeti, ni katika eneo lake katika Jimbo la Ndanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa ni kwamba katika Bajeti hii pia tumezingatia ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. Ni imani yangu maeneo ambayo ameyataja yatakuwemo ili kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo la maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nilitaka niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kumekuwa na malalamiko juu ya ongezeko la bili za maji katika Kata ya Isaka, Kata ya Bugarama; je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuunda tume na niombe au Waziri mwenyewe husika uweze kufika katika Kata ya Bugarama na Kata ya Isaka, ili kuweza kubaini nini chanzo cha ongezeko la gharama za maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kuna fedha iliyobaki katika mradi ambao unatoka Kagongwa – Isaka; je, Serikali ina mpango gani wa kutumia fedha hizo kuweza kuanza kusambaza maji katika Kata ya Mwakata? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Iddi kwa kazi kubwa, nzuri anayoifanya katika Jimbo lake la Msalala, lakini kubwa ambalo nataka kulisisitiza ni haki ya mwananchi wa Tanzania kupatiwa maji na mwananchi naye asisahau kwamba ana wajibu wa kulipia bili za maji. Sisi kama Wizara ya Maji tutasimamia bili hizo zisiwe bambikizi. Tumetoa maelekezo mahususi kwa Taasisi ya EWURA yenye jukumu la kuidhinisha bili za maji na ripoti wamenikabidhi hivi karibuni, tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu swali lake la pili, tunakiri kuna fedha ambazo zimebaki katika mradi wa Isaka – Kagongwa. Tumetoa maelekezo mahususi kwa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira - Kahama, kufanya kazi ile kwa force account kuhakikisha vijiji vyote ambavyo vimebaki vipatiwe huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza, ahsante sana.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; nilikuwa naomba kuuliza ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa Mradi wa Maji ya Kikafu ambao unalenga kuhudumia Kata ya Masama Kusini, Muungano, Bomang’ombe na KIA? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Hai, kiukweli amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana, ni mradi ambao amekuwa akiupigia kelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa tumekwishatoa kibali na tumetoa maelekezo kwa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira - MUWSA, Moshi kuhakikisha kwamba anatangaza kazi hiyo na mkandarasi apatikane mara moja kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, nikiwa mwakilishi wa Jimbo la Kawe mwaka 2010 mpaka 20 tulifanikiwa kwa kiwango kikubwa sana kupunguza tatizo la maji, lakini kuna kata kadhaa ambazo zimebaki bado ni sugu sana. Kata ya Wazo, hususan maeneo ya Nyakasangwe, Mivumoni, Salasala, Kata ya Mbezi Juu eneo la Mbezi Mtoni na Sakuvede. Sasa nataka tu commitment ya Waziri ni lini changamoto hii itafikia ukingoni? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nijibu swali na ninashukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa kukiri kwamba kuna jitihada kubwa ambayo Serikali imefanya katika Jiji la Dar es Salaam na nikiri bado kuna changamoto katika eneo la Mivumoni na maeneo ambayo ameyataja ya Wazo, lakini kuna kazi kubwa ambayo inafanywa juu ya utandazaji wa miundombinu na usambazaji wa maji inayofanywa na DAWASA, zaidi ya kilometa 1,600 ambazo tutaenda kutekeleza. Nataka nimhakikishie sisi kama Wizara tutasimamia kuhakikisha maeneo haya yanapata maji kwa haraka na wananchi waweze kupata maji, ahsante. (Makofi)
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri. Naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali ilitenga fedha kujenga visima nane vya maji katika Wilaya ya Chunya katika Kata za Sangambi, Shoga, Matunda, Skambikatoto, Rualaje, Nkung’ungu na Soweto mpaka Itumbi, lakini mpaka sasa hivi fedha hizo hazijatoka.

Je, ni lini fedha hizi zitatoka ikiwa imebakia takribani siku 40 mwaka huu wa fedha uishe?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwenye chanzo cha maji cha Chunya Mjini kuna takribani visima nane vilichimbwa, lakini visima viwili pekee ndivyo vinavyofanya kazi.

Je, ni kwa nini visima hivi vingine, takribani sita, havifanyi kazi?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Mbarali kuwa miongoni mwa Wabunge ambao wamepitisha bajeti yetu na kutupatia fedha zaidi ya shilingi bilioni 680. Kwa hiyo, jukumu letu sisi kama Wizara ni kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu fedha ambazo kwa ajili ya uchimbaji wa hivyo visima; nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya Saa 07:00 naomba tukutane ili tuweke commitment ya Wizara tuweze kuku-support kuhakikisha wananchi wako wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu suala zima la visima pale katika eneo la Chunya Mjini, kuna visima nane, viwili vinafanya kazi. Nimetoa maelekezo mahususi. Wizara ya Maji inafanya mageuzi makubwa katika kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama kama Mheshimiwa Rais maelekezo yake ametupatia sisi Wizara ya Maji. (Makofi)

Kwa hiyo, maelekezo ambayo tumeyatoa kwamba, kwa wataalam wetu wote kusimamia na kufuatilia, hususan aidha visima ama miradi ya maji, kuhakikisha vyote vinafanya kazi na wananchi waende kupata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipatia nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Muleba iko pembezoni mwa Ziwa Victoria, lakini inalo tatizo kubwa la uhaba wa maji na tunao mradi mkubwa ambao usanifu na upembuzi yakinifu umekamilika.

Je, ni lini sasa Serikali itaanza kujenga mradi wa kutoa maji Ziwa Victoria kwa ajili ya kata sita za Wilaya ya Muleba; Kata ya Gwanseri, Kata ya Muleba Mjini, Kata ya Magata Karutanga, Kikuku, Kagoma na Buleza?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Muleba kwa namna bora na nzuri ambayo kwa kufuatilia wananchi wake waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa ambalo sisi kama Wizara na Bunge lako tukufu, sisi kama Wizara ya Maji tumesema hatuna sababu tena ya Watanzania kulalamika suala la maji. Mwenyezi Mungu ametupa rasilimali toshelevu, tuna rasilimali ya maji mita za ujazo zaidi ya bilioni 126. Tuna mita za ujazo bilioni 105 juu ya ardhi ikiwemo mito pamoja na mabonde na bilioni 21 ambayo iliyokuwa chini ya ardhi.

Kwa hiyo, mkakati ambao tumeuweka sisi kama Wizara na katika bajeti yetu kutumia maziwa, rasilimali toshelevu, kuhakikisha kwamba tunatatua tatizo la maji na moja ya maeneo ambayo ya kipaumbele ni vijiji ambavyo vipo kandokando ya mito ama maziwa. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, sisi ni Wizara ya Maji si Wizara ya ukame. Tunakwenda kutatua tatizo la maji kwa wananchi wako, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mradi wa chujio wa Maswa, Kata ya Zanzui, umeshakamilika na mradi ule unategemewa kusambaza maji katika vijiji kumi, Maswa Mashariki vijiji vitano na Maswa Magharibi vijiji vitano.

Ni lini sasa maji yale yatasambazwa ili wananchi wa Maswa na akinamama wa Maswa wapumzike na adha ya maji? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, kwa kweli anatosha mpaka chenji inabaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa namna nyingine ambayo nataka kusema wananchi wa Maswa changamoto kubwa sana lilikuwa ni chujio kwamba wanapata maji, lakini sio safi na salama na yenye ubora. Kwa hiyo, tumepata fedha, chujio lile tumelikamilisha kazi iliyobaki na ninatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa pale na tumekwishamthibitisha, kipimo chake cha kwanza ni kuhakikisha maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyaeleza kuhakikisha wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama Wizara tutampatia fedha kuhakikisha kwamba anatimiza majukumu yake na wananchi wanapata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; kwa kuwa Jimbo la Kibamba sasa changamoto yake kubwa ni usambazaji wa mabomba tu katika maeneo mbalimbali. Je, Serikali sasa iko tayari kutoa kauli au maelekezo ya utoaji wa mabomba yale ili wananchi wa maeneo mengi wapate maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kidhati ya moyo nikupongeze sana kaka yangu Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Mtemvu. Moja katika bajeti yako umeonesha masikitiko yako eneo ambalo halina maji na tumekwishakubaliana na commitment yangu mimi baada ya Bunge tunakwenda Kibamba tunakwenda kumaliza kabisa tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na tumeshatoa maelekezo mahususi kwa DAWASA, wamefanikiwa maeneo mengi sana, walipe kipaumbele Jimbo la Kibamba katika kuhakikisha kwamba, tunaenda kumaliza kabisa tatizo la maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na nishukuru majibu ya Naibu Waziri. Waziri Mheshimiwa Mbarawa akiwa Waziri wa Maji alipofika kwenye mradi huu aligundua shida ni mfumo ambao ni umeme wa kutumia jua na kwa sababu huo mradi wa REA bado haujaanza kufanya kazi Kata ya Kabwe, ni lini watashirikiana na Wizara ya Nishati ili wananchi wa Kijiji cha Odachi, Kabwe Camp pamoja na Kabwe Asilia waweze kupata maji? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri wangu kwa namna nzuri anavyojibu maswali. Sisi Mawaziri viongozi wetu wametuelekeza kufanya kazi kwa pamoja na tumeshafanya mawasiliano na Mheshimiwa Waziri wa Nishati kuainisha maeneo yote yenye miradi yenye mfumo wa jua kuhakikisha kwamba tunafanya mageuzi kuweka mfumo wa REA kwa maana ya nishati ya umeme ili kuhakikisha kwamba tunapunguza gharama ya uendeshaji ili wananchi waweze kupata huduma ya majisafi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Aida hili jambo tumeshakaa na tumeshaainisha kwa hiyo wenzetu wa nishati watatupa nguvu kuhakikisha maeneo yote yenye solar tunafanya mabadiliko kuhakikisha kwamba tunaweka nishati ya umeme. Ahsante sana.
MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Namuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, kwenye jibu lake la msingi la swali la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Mjini Mpanda amezungumzia chanzo cha maji cha Bwawa la Milala. Bwawa la Milala linaweza likatoa maji kwa muda wa miezi minne tu.

Je, haoni kwamba, itakuwa ni kupoteza pesa kuwekeza katika chanzo ambacho kitatumika kwa muda wa miezi minne tu badala ya kwenda moja kwa moja kuchukua maji kwenye Ziwa Tanganyika? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru, lakini nimpongeze sana sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa namna anavyojibu maswali vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ina rasilimali toshelevu zaidi ya bilioni 126 mita za ujazo. Sasa mkakati wa Wizara ni kutumia rasilimali toshelevu kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya majisafi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ambaye ni Waziri wangu ambaye amenifunza mpaka leo nipo hapa, hili jambo tunalizingatia katika kuhakikisha kwamba wananchi hawa tunaenda kuwaondolea tatizo hili. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza nashukuru kwa majibu mazuri yenye matumaini yaliyotolewa na Mheshimiwa Waziri kwa wananchi wa maeneo ambayo walikuwa na shida kubwa ya maji, lakini pamoja ma majibu hayo mazuri naomba kuuliza Mheshimiwa Waziri kwamba kwa kuwa katika Kata za Mpanyani, Namatutwe, Msikisi, Namajani ambao pia Nambawala ipo katika Kata ya Mpanyani, wananchi hawa hawajawahi kuona maji salama kwa maana ya mabomba na naomba kuuliza; je, Serikali ina mpanga gani wa kuharakisha uchimbaji wa mabwawa katika kata hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Kijiji cha Mraushi na vitongoji vyake ambapo katika majibu ya msingi Serikali imethibitisha kwamba ujenzi wa mradi wa kuwapatia maji wananchi hao umeanza kwa bajeti ya mwaka 2021/2022. Ni lini mradi huo utakamilika ambapo pia nina uhakika Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kuambatana na mimi kwenda kujionea kadhia ya hali ya maji katika maeneo hayo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake mkubwa na si mara moja amekuja katika Wizara yetu ya Maji kuhakikisha wananchi wake kuwa wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, kwanza nilishukuru sana Bunge lako Tukufu sisi Wizara ya Maji kutuidhinishia zaidi ya shilingi bilioni 680. Lakini kwa namna ya kipekee Mheshimiwa Rais kwa dhamira yake njema ya kuhakikisha kwamba anakwenda kumtua mwana mama ndoo kichwani ametupatia fedha ya nyongeza zaidi ya shilingi bilioni 207; haijawahi kutokea; nataka nimuhakikishie fedha zile moja ya mipango ni kuhakikisha kwamba tunakwenda kununua vitendea kazi kwa maana ya magari ya kisasa kwa ajili ya ujengaji wa mabwawa pamoja na uchimbaji wa visima. Kata zake alizoainisha tutakwenda kuzipa kipaumbele katika kuhakikisha kwamba tunakwenda kutatua tatizo la maji. Ahsante sana.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye Wilaya ya Kyerwa kuna mradi wa vijiji 57, mradi huu Serikali imesema utajengwa kwa awamu, lakini kwenye bajeti kuna Kata ya Kikukulu, Kata ya Songembele, Kichwechwemkula na Rukaija havikuwekwa bajeti. Nini kauli ya Serikali juu ya kata hizi ambazo hazikuwekwa kwenye bajeti? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Bilakwate kwa namna anavyopigania jimbo lake la Kyerwa, kubwa ambalo nataka nimuhakikishie mkakati wa Wizara yetu ya Maji ni kuhakikisha tunatumia vyanzo toshelevu ikiwemo Mto Kagera.

Sasa moja ya vijiji ambavyo vingi tunakwenda kutatua tatizo la maji zaidi ya 50. Tumesema mradi huu tunakwenda kuutekeleza kwa awamu, kata ambazo hazipo katika bajeti hii tutahakikisha bajeti ijayo tunaziweka ili kuhakikisha kwamba wananchi wake wanaweza kupata huduma hii muhimu ya maji. Ahsante sana.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri na jitihada za Serikali ambazo imefanya. Nashukuru kwa mpango wa muda mrefu, lakini mpango wa muda mrefu utachukua muda mrefu, sasa kwa mpango wa muda mfupi pale kwenye Mto Mantengu pale Vwawa; iwapo mnaweza kufunga pump mbili zenye uwezo wa kusukuma maji tunaweza tukapunguza upungufu wa maji katika Mji wa Vwawa kwa kiwango kikubwa.

Sasa je, ni lini Serikali itakuwa na mpango wa kufunga pump mbili kubwa za kuweza kusukuma maji katika katika Mto Mantengu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Rais wa Awamu ya Tano alipotembelea Mji wa Vwawa mwaka 2019 alitoa shilingi milioni 100 na ndio zikaenda kuchimba visima vitatu katika eneo la Ilolo, Old Vwawa na Naihanda. Lakini visima hivyo vilitelekezwa mpaka leo bado havijafunga miundombinu.

Sasa je, Mheshimiwa Waziri utakuwa tayari kuambatana na mimi baada ya kipindi hiki cha Bunge ili twende tukaangalie hali halisi na tutatue changamoto ya muda mrefu ya wananchi wa Mji wa Vwawa? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ukimuona mtu mzima analia ujue kuna jambo. Sasa nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge maji hayana mbadala na kwa kuwa tukiweka ama tukifunga pump mbili wananchi wako wanakwenda kupata maji toshelevu, nikuombe baada ya saa Saba tukutane tutoe fedha kuhakikisha kwamba pump zile zinapatikana na wananchi wako wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, nipo tayari kuongozana na wewe Mheshimiwa Mbunge kuhakikisha kwamba tunakwenda kukulindia jimbo lako la Vwawa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Wilaya ya Rungwe katika Kijiji cha Masukulu kumekuwa na shida sana ya maji japokuwa Serikali ilipeleka fedha. Je, hamuoni kuna haja ya kutuongezea fedha ili maji yaweze kuenea katika vijiji vinavyozunguka Kata ya Masukulu?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, lakini kubwa ambalo nataka nimuhakikishie, Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, dhamira yake kumtoa mwana mama ndoo kichwani, kwa hiyo sisi tupo tayari kutoa fedha kuhakikisha wananchi wako wa Masukulu wanapata huduma ya maji sasa.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika ahsante kwa kunipa nafasi, Wilaya ya Wanging’ombe kuna Mradi wa Maji wa Igando - Kijombe wa shilingi bilioni 12 ulitakiwa uwe ushakamilika tangu mwaka 2019 lakini hadi sasa hakuna kitu kinachoendelea. Nilitaka kujua lini Serikali itakamilisha mradi huu?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, sawa na nataka niseme tu unatosha mpaka chenji inabaki, lakini kubwa ambacho ninachotaka kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha, sasa sisi tumeshapatiwa fedha kuhakikisha kwamba tunakamilisha miradi mbali mbali, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaupa nguvu mradi wake, kuhakikisha tunapeleka fedha kwa wakati, ili mradi ukamilike na wananchi waweze kupata huduma maji safi na salama.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ulikuwa wananchi wa Kata za Goweko, Kigwa, Nsololo na Igalula kupata maji Desemba, 2021 lakini majibu ya Serikali yamekwenda tena Juni, 2022. Lakini utekelezaji wake mpaka sasa hivi umefikia asilimia 10.

Je, Serikali haioni kuusogeza karibu mradi huu uweze kutekelezeka kwa kasi ili wananchi wa kata hizo waweze kupata maji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Jimbo la Igalula lina changamoto sana ya upatikanaji wa maji, ndiyo maana tunaelekeza Serikali iwekeze katika uchimbaji wa mabwawa. Niiombe Serikali haioni haja ya uharakishaji wa haraka wa usanifu wa uchimbaji wa mabwawa hasa hili Bwawa la Kizengi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Igalula kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya. Ni Mbunge mfuatiliaji, mpambanaji hususan katika suala zima la wananchi wake waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Nitoe shukrani kwa Bunge lako tukufu kwa kutuidhinishia fedha zaidi ya bilioni 680 lakini Mheshimiwa Rais naye ametupatia fedha ya nyongeza zaidi ya bilioni 207. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge maeneo ambayo tutayapa kipaumbele na kuyapa fedha za kutosha ili kukamilisha mradi ule ni eneo la mradi huu wa Igalula kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na wananchi wake wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara yetu ya maji tumeboresha Kitengo chetu cha Uchimbaji wa Mabwawa. Tunaona kabisa yapo maeneo ambayo hayana fursa ya uchimbaji wa visima. Tunataka maji ya mvua isiwe laana, tunataka tuyavune kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa ili Watanzania waweze kunufaika na uvunaji wa maji ya mvua waweze kupata huduma ya maji.

Kwa hiyo, mkakati uliokuwepo tunakwenda kununua seti ya ujenzi wa mabwawa kwa maana ya vitendea kazi ili kazi hii ianze na Watanzania waweze kunufaika na ujenzi wa mabwawa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona nami kuuliza swali la nyongeza.

Kwanza nishukuru Serikali kwa kuanzisha RUWASA, lakini pamoja na hayo RUWASA inakabiliwa sana na tatizo la upungufu wa wataalam pamoja na vitendea kazi.

Je, Serikali ina mkakati gani katika kutatua tatizo hilo ili kuleta ufanisi wa utendaji kazi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kutambua umuhimu wa uanzishwaji wa Wakala wa Maji Vijijini - RUWASA; hili nipendekezo lenu Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, kikubwa ambacho tulianzisha RUWASA kwa minajimu ya kwenda kutatua tatizo la maji vijijini. Ipo changamoto hususan ya watumishi. Tumeomba kibali kupitia Ofisi ya Rais - Utumishi kuhakikisha kwamba tunapata watumishi wa kutosha. Lakini katika kipindi hiki maelekezo ambayo tumeyatoa Wizara ya Maji kuhakikisha kwamba tuna Mamlaka za Maji kule mikoani waungane kwa pamoja ili katika kuhakikisha kwamba wana team up ili kuhakikisha kwamba miradi inakwenda na Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji katika Kata ya Mnazi, Tarafa ya Umba ni takribani miezi miwili sasa RUWASA wamepeleka saruji na mipira ile midogo, lakini mpaka sasa tunasubiri mabomba. Ni lini mabomba haya yatapelekwa ili maji katika Mji wa Mnazi na viunga vyake yaweze kupatikana kwa urahisi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Shangazi, kaka yangu ambaye anafanya kazi kubwa sana katika Jimbo lile la Mlalo.

Mheshimiwa NaibU Spika, nataka nimhakikishie maji hayana mbadala na sisi kama Wizara ya Maji umuhimu wetu na jukumu letu ni kuhakikisha tunalinda uhai wa wana Mlalo na wana Mnazi. Natoa maelekezo kwa Mhandisi wa Maji wa pale Lushoto kuhakikisha mpaka Jumatatu mabomba yamefika na kazi ianze mara moja. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu SPika, maji ni uhai kwa viumbe vyote, maji ni muhimu kwa ustawi.

Naomba kuuliza swali langu, Jimbo langu la Mchinga halina maji safi na salama. Sasa ningeomba jimbo hili lifikiriwe kwa umakini mkubwa kupata maji safi na salama kutoka chanzo kikubwa cha Ng’apa.

Je, ni lini maji safi na salama ya bomba yatapelekwa katika Jimbo langu la Mchinga kwa ajili ya wananchi wa jimbo hilo? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, dhati ya moyo kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Mama yangu Salma Kikwete, kiukweli ni Mbunge ambaye kwanza anajua changamoto za watu wake na anaelala na mgonjwa ndiye anayejua mihemo ya mgonjwa. Kwa hiyo, naomba nimpe upendeleo maalum kabisa moja kufika kwanza katika jimbo lake la Mchinga, lakini la pili tunatambua kweli tuna chanzo toshelevu pale Ng’apa ambapo tumejenga mradi ule wa Lindi. Tunataka tuyatoe maji ya pale Ng’apa ili kuhakikisha kwamba yanafika katika Jimbo la Mchinga ili wananchi wa Mchinga waweze kuondokana na tatizo hilo la maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bwawa la Ichemba lililopo katika Kata ya Ichemba lilikuwa kwenye mpango wa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2015 lakini mpaka dakika hii halijawekwa kwenye huo mpango na baada ya kuingia RUWASA hilo bwawa limesahaulika kabisa. Tunajua bwawa hilo likikamilika linakwenda kutatua kero katika kata tisa za Jimbo la Ulyankulu.

Je, ni lini bwawa hili sasa litawekwa katika mpango wa upembuzi yakinifu na kukamilika kwa ujenzi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge na nimpongeze sana; katika kipindi ambacho tunaenda kuandika historia katika Wizara yetu ya Maji ni kipindi hiki kwa sababu Mheshimiwa Rais amedhamiria kwa dhati kabisa. Wanasema, yafaa nini imani bila matendo? Mheshimiwa Rais ametuongezea fedha zaidi ya shilingi bilioni 207 kwa ajili ya kwenda kutatua matatizo ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, maeneo ambayo tutawapa kipaumbele ni maeneo yale yenye changamoto na ninatambua Ulyanhulu ni maeneo ambayo yana changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaunga mkono na tutatoa fedha kuhakikisha ile kazi inaanza na wananchi wako waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa tatizo la maji katika Jiji la Dar es Salaam kwenye Jimbo langu la Kawe hasa Kata ya Wazo kwenye eneo la Madale, Kisanga, Mbezi Juu hakuna maji kabisa. Waziri anasemaje kwa habari ya kuwapa maji watu wa Kawe, ni lini hasa Mheshimiwa Waziri? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, brother wangu Gwajima kwa kazi kubwa ya muda mfupi ambayo anaifanya katika Jimbo lile la Kawe. Tarehe 5 Julai nitakuwepo Jijini Dar es Salaam nina mazungumzo na watu wa DAWASA.

Mheshimiwa Mbunge nikuombe uwepo katika kikao kile na moja ya maelekezo ya haraka tutakayoyafanya ni kuhakikisha wananchi wa Wazo wanaenda kupata maji kwa haraka. Ahsante sana.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu za Serikali zinaonesha kwamba maji vijijini yanapatikana asilimia 74 na mijini ni asilimia 85 kwenda 90; lakini uhalisia unaonesha kwamba mnasema watu wamepata maji kutokana na kuweka miundombinu na sio nyumba kwa nyumba.

Kwa kuwa sasa hivi tunaenda kwenye sensa ya Taifa ambapo watu wataenda kufanyiwa hesabu nyumba kwa nyumba. Kwa nini msitumie utaratibu huu wa sensa ili kuweza kupata takwimu halisi ya kila nyumba ambayo inapata maji nchi hii? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze na nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge dada yangu Halima, sisi Wizara yetu ya Maji inafanya mageuzi makubwa sana na moja ya eneo ambalo eneo unalizungumzia sisi tumeshalifanyia kazi. Tumekutana na watu wetu wa takwimu ili kuhakikisha kwamba tunakwenda kwenye hilo hilo. Lakini tunataka tujiongeze mbali zaidi. Badala ya kusema tu asilimia ngapi watu wanapata maji, tunataka twende mbali zaidi, tunataka tujue Tanzania kuna vijiji vingapi, vingapi vimepata maji, vipi havijapata maji ili tuhakikishe tunaviongezea nguvu maeneo ambayo hayana maji ili waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Licha ya majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwanza niishukuru Serikali, nina furaha sana kuona kuwa Mradi wa Chagongwe, ambao ni wa muda mrefu, unaanza. Je, mradi huu wa kutoka Milima ya Chagongwe na Nongwe utaanza kutekelezwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Manispaa ya Morogoro, nashukuru Serikali inaendesha miradi ya maji kwenye manispaa yetu, lakini hata hivyo bado tunapata maji ya mgao. Je, miradi hii, hasa mradi wa Bwawa letu lile la Mindu, ni lini hasa litakamilika na miradi mingine, ili wananchi wa manispaa waweze kupata maji kila siku na waondokane na maji ya mgao? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge mama yangu Dkt. Christine Ishengoma ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa kazi kubwa na nzuri na anatusimamia vizuri sana ili sisi Wizara kuhakikisha watu wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge, ambacho ninataka kukuhakikishia Mheshimiwa Mwenyekiti wetu ni kwamba eneo la Mradi huu wa Chagongwe, katika mwaka huu wa fedha tunaokwenda nao tumepata fedha ambazo ni za ziada za Mheshimiwa Rais, zaidi ya bilioni 207. Hili ni eneo ambalo tutalipa umuhimu mkubwa kuhakikisha katika mwaka huu unaoanza wa fedha, kwenda kuanza mradi huu na wananchi wa Gairo waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la Mheshimiwa Mbunge ni kuhusu suala zima la maji katika eneo la Morogoro. Mji wa Morogoro uzalishaji wake ni lita milioni 35, lakini mahitaji yake kwa sasa ni lita milioni 67, kwa hiyo, kuna uhitaji mkubwa sana wa maji, kwa hiyo mkakati wa haraka katika siku 100 za Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan, ametupatia fedha zaidi ya bilioni nne kwa ajili ya kujenga mradi wa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, na tumejenga tenki la lita milioni mbili eneo la Mgulu wa Ndege ambapo tutakwenda kutumia chanzo cha maji cha Mambogo ambao tumeweka maji katika tenki lile la Mgulu wa Ndege ambapo maji yale yatakwenda Kihonda, maji yale ambayo yatakwenda eneo la SGR, Lukobe na Mkundi katika ili kuhakikisha wananchi wa Morogoro wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mkakati wa kumaliza kabisa tatizo la maji katika Mji wa Morogoro, tumepata fedha zaidi ya Euro milioni 70, ambapo tumekwishasaini mkataba na wahandisi washauri, mradi ule tunakwenda kuhakikisha unaanza kwa haraka ili wananchi wa Morogoro waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nami nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itajenga na kuboresha miundombinu ya maji katika Jimbo la Muhambwe, hususan Kata za Kibondo Mjini, Bunyambo na Kitahana ili kukabiliana na uhaba mkubwa wa maji ulioko katika jimbo hilo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe, nadhani mwezi mmoja ama miwili iliyopita, Mheshimiwa Mbunge wa Mihambwe ameingia katika Bunge hili. Amekuja ofisini, na jana tumekwisha mpa pesa, zaidi ya milioni 100 ili kuhakikisha kwamba wananchi wake wanakwenda kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii. Chanzo cha maji ya Mitema ambacho kipo katika Jimbo la Newala Vijijini kina maji ya kutosha kiasi kwamba kama uwekezaji wa fedha utakuwa wa kutosha, tatizo la maji katika Jimbo ya Newala Vijijini, Newala Mjini, Tandahimba na baadhi ya Kata za Nanyama zitaondokana na shida ya maji. Je, ni lini Serikali itawekeza fedha za kutosha katika chanzo cha maji cha Mitema ili kuondoa kadhia ya maji kwa wananchi wa maeneo tajwa? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Newala Vijijini. Lakini pia nimpongeze sana, juzi tuliweza kukutana pia na Mheshimiwa Mbunge wa Newala Mjini, baba yangu, mzee wangu, Mheshimiwa Kapteni Mkuchika, juu ya Mradi huu wa Makonde. Ni mradi wa muda mrefu sana ambao umekuwa na maneno mengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwahakikishie nikiwa mwenye dhamana ya Wizara ya Maji, Mheshimiwa Rais ametupa maelekezo mahususi kwa ajili ya Watanzania, waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Juzi tumekaa kikao baada ya mazungumzo yale, maelekezo ambayo tumeyatoa ni kwamba mradi ule tunakwenda kuuanza, iwe jua iwe mvua, ili wananchi wa Newala waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa Waziri wa Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachosema ni kwamba Sengerema tunadaiwa pesa, shilingi milioni 300 kwa ajili ya umeme, na hili deni limekuwa la muda mrefu. Nini kauli ya Waziri kuhusiana na deni hilo ili tuanze kuanza upya, kwa sababu tumepata meneja mpya Sengerema? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Sengerema kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Ni haki ya mwananchi kupatiwa huduma ya maji. Na mwenye wajibu na jukumu la kumpatia huduma ya maji ni Wizara ya Maji, kwa maana ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sengerema ni eneo ambalo lilikuwa na changamoto sana ya maji. Serikali kwa dhamira
njema imewekeza mradi wa zaidi ya bilioni 25 wananchi wa Sengerema waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Sasa ni jukumu la Mamlaka ya Maji ya Sengerema kuhakikisha kwamba inakusanya bili na kulipia umeme ili uendeshaji wake uwe vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tuna changamoto ya uendeshaji; Meneja, kwa maana ya Mkurugenzi wa mamlaka ile nimemuondoa, fedha hizi za deni tutazilipa, lakini kwa masharti ya kuhakikisha kwamba wanajitegemea na wanaendesha mamlaka ile vizuri na wananchi wa Sengerema wanapata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, kumekuwepo na tatizo kubwa la kukatika sana kwa maji katika Mji wa Munze, Kishapu, Kata ya Mwadui Lohumbo, na Maganzo. Lakini Mheshimiwa Waziri aliwahi kujibu kwamba tatizo kubwa ni malipo ya madeni ya muda mrefu ya wateja, lakini wateja wamelipia madeni yao kwa wakati. na hili nimefuatilia mwenyewe nimeona kwamba kweli hawadaiwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufika katika Jimbo la Kishapu kujionea na kutoa utatuzi wa kudumu juu ya tatizo la kukatika kwa maji katika Mji wa Munze na maeneo mengine?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana kaka yangu, Mbunge wa Kishapu; kwa kweli unafanya kazi kubwa na nzuri sana katika jimbo lako.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niweke wazi kabisa maeneo ambapo Serikali imewekeza miradi mikubwa kwa
ajili ya wananchi waweze kupata huduma ya maji, na wananchi wanalipia bili za maji ili kuhakikisha kwamba mamlaka inajiendesha, maeneo ambayo wananchi wanalipia bili zile za maji lakini wakurugenzi ama watendaji ambao wanashindwa kuendesha mamlaka hizo, hakuna neno lingine zaidi ya kutupisha. Tutaweka watu ambao wataweza kutuendesha ili mamlaka zetu ziweze kwenda na Watanzania waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Ahsante sana.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa kumtua mama ndoo kichwani mradi mkubwa ambao utasababisha hili litokee ni mradi wa Miji 26 ambao unafadhiliwa na Serikali ya India. Tunaomba kuuliza Mheshimiwa Waziri.

Ni lini mradi huu utaanza na umefikia wapi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge lakini kama unavyotambua program ya kumtua mwana mama ndoo kichwani ni programu ya Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ya maji kupitia bajeti ya Serikali lakini kupitia wadau mbalimbali wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Serikali ya India tunatarajia kutekeleza miradi ya Miji 28 zaidi ya dola milioni 500 na mpaka sasa hatua ambayo tumefikia taratibu zote za kimanunuzi kama Wizara ya Maji tumeshazikamilisha. Tunasubiri kibali (no objection) kutoka Exim Bank na hivi karibuni tutapata, katika kuhakikisha tunatekeleza miradi hiyo na wananchi waendelee kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. SAMWEL X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Changamoto ya maji inayoikumba Jimbo la Mwibara ni sawasawa na ambayo tunaipata kwenye Mkoa wetu wa Manyara na sehemu kubwa huwa tunapata changamoto kubwa hasa kwenye eneo la kuchelewa kwenye suala la manunuzi. Pale Mkoani hatuna Afisa Manunuzi.

Je, Wizara iko tayari kwa kushirikiana na Utumishi kupeleka Afisa Manunuzi pale Mkoani ili kuharakisha manunuzi? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Hanang kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Jimbo lake. Sisi kama Wizara ya Maji tutaendelea kumpa ushirikiano katika kuhakikisha tunatatua matatizo ya maji katika Mkoa wa Manyara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la Maafisa Manunuzi ni kweli tumeanzisha Taasisi yetu ya (RUWASA) Wakala wa
Maji Vijijini, hii ni mahususi kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji vijijini. Lakini tumekuwa na changamoto ya watumishi hususani katika eneo la manunuzi. Tumeshafanya mazungumzo na wenzetu wa Utumishi na hivi karibuni tutapata Maafisa hao katika kuhakikisha tunakwenda kutatua matatizo ya maji. Eneo ambalo tutalipa kipaumbele kabisa ni Mkoa wa Manyara katika kuhakikisha hii changamoto tunaifanikisha kwa haraka. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa moyo wa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Aweso, kwetu sisi amejitahidi kuutendea haki Mradi wa Bunda umepiga hatua. Sasa ningependa kuuliza swali la nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maji yametoka Nyabehu yamekuja Bunda Mjini. Katika mkataba wa ule mradi ilikuwa ni pamoja na kujengwa vituo. Hivi tunavyozungumza bado vituo havijajengwa Kata tu ya Gutagushigwamara hakuna kituo. Nyabeu yenyewe kiko kimoja, ukienda Kinyambwiga hakuna kituo, ukija Bunda Store huku hakuna kituo. Manyamanyama, Nyasura, Sazila hayo maeneo yote kama kungejengwa vituo tungeweza kupata maji katika Kata zote 14 kwa huo mradi uliochukua zaidi ya miaka 13. (Makofi)

Sasa kwa mujibu wa ule mkataba ni lini sasa hivyo vituo vitakamilika ili wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Bunda Mjini wasahau biashara ya kupata shida ya maji safi na salama? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Lakini nataka nimuhakikishie sisi kama Wizara ya Maji tumefanya mageuzi makubwa sana, kupitia Wizara yetu ya Maji na Rais wetu support kubwa ambayo anatupa ya kifedha. Tulikuwa na miradi kichefuchefu zaidi ya 177 asilimia nyingi tumekwisha ikamua. Sasa nataka nimpe mwaliko mahususi kabisa tarehe 7 Mheshimiwa Rais wetu mpenzi Mama Samia Suluhu Hassan atakuwepo Bunda. Naomba tujumuike ukaone kazi kubwa na nzuri ambayo imefanywa na Wizara yetu ya Maji katika Jimbo lako. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Matatizo yaliyoko katika Jimbo la Mwibara na maeneo mengine ya Tanzania, yanafanana kabisa na matatizo yanayopatikana katika Jimbo la Kigoma Kaskazini. Ndani ya Jimbo la Kigoma Kaskazini tuna mradi wa Mkongoro I, ambao umechukua muda mrefu na huu mradi unakwamisha adhima ya Mheshimiwa Rais ya kumtua ndoo mama kichwani.

Naomba kujua ni lini huu mradi utaukamilisha ili tuweze kuwasaidia mama zetu katika Jimbo la Kigoma Kaskazini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge na nimeshafika katika Jimbo lake kiukweli unafanya kazi kubwa, unafanya kazi nzuri kama kijana. Sisi kama Wizara ya Maji tutaendelea kukupa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wizara yetu ya Maji tumesema miradi ambayo imetumia kwa muda mrefu mkakati wetu ni kuhakikisha tunaikamilisha. Nikuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge saa 7.00 tukutane tuone namna gani ya ku-push mradi ule ili tuweze kuukamilisha. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali moja la nyongeza, nashukuru kwa majibu mazuri sana ya Serikali na niruhusu vile vile kumpongeza kidhati Mheshimiwa Jumaa Aweso Waziri wa Maji kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya katika kutekeleza miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi hizi na shukurani hizi vile vile zimfikie Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kumuamini kwenye Wizara hii. Ninaamini wale ambao huwa wanapita pita kutoa zile PhD kama za Dkt. Musukuma punde tu watampa Udaktari wa Miradi ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa majibu haya mazuri na kwa ahadi ya Serikali ya kufikia Mwezi Agosti, 2022 miradi hii itakamilika je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kuambatana na Mheshimiwa Mnzava kufanya ziara punde tu baada ya Bunge hili?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana kaka yangu Jerry Silaa kwa kazi kubwa ambayo anayoifanya, katika Jimbo lake la Ukonga kwa kweli anafanya kazi kubwa na nzuri sana na yenye kuonekana. Lakini kubwa kuhusu suala la kwenda katika Jimbo la Mkoa wa Shinyanga niko tayari baada ya Bunge hili. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa nafasi ambayo amekuwa akinipa kujadili miradi ya Wilaya ya Kyerwa.

Swali langu la nyongeza, tunao mradi wa vijiji 57 na mradi huu Mheshimiwa Waziri tumekubaliana unajengwa kwa awamu. Lakini kuna mradi unaotoka Kyerwa, Nyaruzumbula, Nyakatuntu mpaka Kamuli. Mradi huu umechukua muda mrefu ni lini mradi huu utaanza? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote dhati ya moyo nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge wa Kyerwa kwa kazi kubwa na nzuri, ambayo anaifanya na amekuwa msumbufu sana kuhusu suala zima la Jimbo lake liweze kupatiwa huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuhakikishie utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan sisi Wizara yetu anatupatia fedha kila mwezi kupitia Mfuko wa Maji na tumetengewa zaidi ya shilingi bilioni 459.2 kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji vijijini. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge ahadi ambazo tuliziahidi kama Wizara ya Maji tutakwenda kuzitekeleza kwa sababu ya upatikanaji wa fedha ambazo tunapewa na Mheshimiwa Rais. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali langu ni dogo kweli na fupi. Sote tunakumbuka wakati wa bajeti hapa Mheshimiwa Waziri aliahidi kwamba ile Miji 26 ya Miradi ya (India) itatekelezeka ndani ya muda. Lakini leo wakati Mheshimiwa Mwanyika anauliza kutaka kujua status ambapo tuna mradi huo wa kutoka Rorya kwenda Tarime Mjini. Tunataka kujua exactly ni lini utakamilika huu mradi? Sio kwamba mtuambie mnasubiri kibali kutoka Exim Bank ni lini utakamilika? Maana yake wananchi wanategemea kupata huduma hii ya maji. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na najua dhati ya moyo namna gani wananchi wako wanataka huduma ya maji. Utekelezaji wa miradi ya maji lazima tukubali upitie taratibu ama michakato mbalimbali ambayo inahitajika. Michakato ya manunuzi sisi kama Wizara ya Maji tumekwishaikamilisha. Tunakamilisha taratibu za manunuzi lazima tupeleke katika Exim Bank ambao wanatupa kibali cha (no objection). Sisi kama Wizara ya Maji tumeshazungumza na wahusika kuna mambo machache ambayo wanayakamilisha na muda si mrefu tutapata kibali kile kwa ajili ya kwenda kutekeleza miradi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge Subira yavuta kheri na kheri itapatikana juu ya utekelezaji wa miradi ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, afadhali. Swali langu moja kwa Wizara ya Maji. Kampuni ya (DDCA) au Wakala wa Kuchimba Visima nchini Wilaya ya Songwe kupitia TARURA Songwe tumewalipa Shilingi milioni 158 tarehe 24 Novemba, 2021 kwa ajili ya kuchimba visima ili tuweze kupata fedha kwa ajili ya miradi ya maji. Lakini mpaka leo Kampuni hiyo haijachimba visima na nimekuwa nikiwasiliana na CEO wa DDCA anakosa majibu na gari lipo lakini hawajaja bado kuchimba visima katika Wilaya ya Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa namuomba Mheshimiwa Waziri ni lini sasa gari hilo litakuja Wilaya ya Songwe kwa sababu Wilaya ya Songwe ni scattered na mvua zimeshaanza kunyesha na kuna baadhi ya maeneo mwezi huu njia ile itakuwa haipitiki kwa sababu ya mvua?

Lakini je, nilikuwa najaribu kumuomba Mheshimiwa Waziri atafute Kampuni nyingine tuweze kuchukua fedha DDCA tuweze kuchimba visima kwa ajili ya kuendeleza miradi ya maji Songwe.
WAZIRI WA MAJI: Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa wa Songwe kaka yangu Mulugo kwa kazi kubwa na nzuri ambayo unaifanya katika Jimbo lako. Nataka nimuhakikishie nikiri Waheshimiwa Wabunge kama mnakumbuka katika Bunge la Bajeti, mlitoa changamoto juu ya utendaji katika suala zima la Wakala wetu wa Maji na Uchimbaji Visima na Mabwawa (DDCA). Tulikuwa na changamoto ya kiutendaji tumeshafanya mabadiliko hususani Mkurugenzi yule ambaye anasimamia Taasisi ile na muda mfupi mtaona mabadiliko hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara ya Maji hatupo tayari kuona wananchi wa Songwe wanateseka ili hali fedha zimeshalipwa. Nikuombe Mheshimiwa Mbunge tukutane tufanye alternative ya haraka katika kuhakikisha visima vile vinachimbwa na wananchi wanufaike na kazi kubwa na nzuri inayofanywa na Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Changamoto iliyopo kwenye Jimbo la Kyerwa inafanana kabisa na changamoto zilizopo Wilaya ya Chemba. Changamoto kubwa ni miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naishukuru sana Serikali kwa kupitia Wizara ya Maji, nami ni shabiki mkubwa wa Mheshimiwa Waziri Jumaa Aweso. Yale maneno ambayo Ndugu yangu Mheshimiwa Jerry Silaa alisema, nami nayathibitisha kwamba anapaswa kupewa zile Ph.D ambazo zinatolewa, tena apewe Tanzania. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu sasa. Pamoja na kuwa tumepata visima vitano na vimechimbwa zaidi ya miaka miwili, vingine mmoja, lakini bado havifanyi kazi kwa sababu miundombinu yake haipo tayari: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua, ni lini sasa Serikali kupitia Wizara ya Maji itaweka miundombinu ili watu wale nao waanze kupata maji? Ahsante sana.(Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, kwa kweli nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge wa Chemba kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa muda mfupi katika Jimbo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni kweli tulishafika Chemba, hali ya Chemba ilikuwa siyo nzuri. Maelekezo ya kwanza ambayo tumeyafanya ni katika kuhakikisha kwamba tunachimba visima vya dharura ili wananchi wa Chemba waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Nataka nimhakikishie katika mfuko wa mwezi huu tutatoa fedha ya uanzaji wa miradi ile ili wananchi wa Chemba waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kumaliza kabisa tatizo la Maji Chemba, siyo maeneo yote ambayo utachimba ukapata huduma ya maji. Eneo la Chemba limetupa experience baadhi ya maeneo yamekuwa na ukame. Tunakwenda kuchimba bwawa kubwa katika kuhakikisha wananchi wa Chemba wanaendelea kunufaika na maji. Tunaona mvua zinazonyesha maji yanapotea tu. Mkakati wa Wizara na mageuzi ya Wizara ni kuhakikisha tunachimba mabwawa makubwa ili kuvuna maji na wananchi wa Chemba waendelee kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nakushukuru kwa kuniruhusu niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la Jimbo la Kyerwa la maji, linafanana sana na tatizo la Jimbo la Kawe; na kwa kuwa ndugu Waziri wa Maji, Mheshimiwa Jumaa Aweso alikuwa na mradi unaotokea Ruvu Chini mahali ambapo amejenga matenki Mabwepande, Bunju A, Tegeta, Salasala na maeneo mengine ya Jimbo la Kawe; na mradi huu ulitegemewa mwisho wa mwaka Desemba uwe umeshakamilika ili watu wapate maji, lakini mpaka leo Madale, Nakasangwe, Kisauke, Mabwepande, Tegeta hazina maji: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini sasa mradi huu utakamilika ili wananchi wangu wa Jimbo la Kawe wapate maji? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, kwa kweli nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, kaka yangu Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima kwa kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo la Kawe. Kwa kweli maeneo ya Mabwepande yamekuwa na changamoto kubwa sana na tunaona kazi kubwa inayofanywa na DAWASA. Naomba baada ya saa 7.00 tukutane, tufanye mawasiliano na Mkurugenzi wa DAWASA ili tuweze kutia nguvu kwa pamoja na mradi ule uweze kukamilika na wananchi wa Mabwepande waendelee kupata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Je, ni lini sharti litawekwa sasa baada ya kutoa mwongozo huo (Building Regulations) ya majengo yote ya Serikali na hata ya watu binafsi kuwa na makingamaji ili waweze kuihifadhi hayo maji ya mvua?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Kwa kuwa maji hayo yanaharibu sana barabara wakati wa masika, hasa maeneo ya mlimani kama ya Wilaya zote za Mkoa wa Kilimanjaro na yanaosha kabisa ile changarawe kwenye barabara: Ni lini mitaro mikubwa itajengwa katika barabara hizo ili iwe salama? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya, lakini kubwa ambalo nataka nimhakikishie kupitia Wizara yetu ya maji tumeshatoa maelekezo na tumekubaliana kwamba mvua isiwe maafa, mvua iwe fursa. Kwa hiyo, moja ya mkakati wetu ni kuwa na ushirikiano na Wizara nyingine, kwa maana ya Wizara ya TAMISEMI. Mwananchi kule anapotaka kujenga nyumba yake, basi uwekwe utaratibu namna gani anaweza kuvuna maji ya mvua ili aweze kuondokana na matatizo ama changamoto ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kikubwa, Wizara ya Maji itashirikiana na Wizara nyingine ikiwemo Wizara ya TAMISEMI ili kuhakikisha wananchi wetu nyumba wanazojenga wanaweka miundombinu ya uvunaji wa mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine, tumeona baadhi ya maeneo mbalimbali mvua inaponyesha inaleta maafa na kuleta athari mbalimbali. Maelekezo ya Mheshimiwa Rais katika Wizara yetu ya Maji ni juu ya ujenzi wa mabwawa ili kuhakikisha kwamba tunavuna maji na kwa kushirikiana na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kujenga miundombinu ili mvua zinaponyesha zisilete athari na badala yake iwe fursa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. AGNES J. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali madogo ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi 2022, idadi ya watu imeongezeka: Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza mawanda ya mradi huo ili kuongeza idadi ya watu watakaonufaika na mradi huo?

Mheshimiwa Spika, pili, chanzo cha maji cha Chiwambo na Maratu havitoi maji kwa sasa kutokana na deni kubwa la bili ya TANESCO. Serikali ina mpango gani wa kusimamia jambo hili ili kuwawezesha wananchi hao kupata maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Hokororo kutokana na kazi kubwa anayoifanya hasa kupigania wananchi wake kwa ajili ya kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; Wizara ya Maji kutokana na takwimu hii ya ongezeko la watu, tumejipanga kutumia kwanza vyanzo toshelevu kwa maana ya mito na maziwa ili kuhakikisha kwamba tunawafikia watu wengi ili kuendelea kutoa huduma ya maji. Mathalani, huu Mradi wa Nanyumbu, tunatoa maji ya Mto Ruvuma ili kuhakikisha wananchi wengi wanaenda kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ipo mamlaka ambayo ina deni na TANESCO. Namwomba Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge tukae ili kuona namna gani tunaweza kuisaidia mamlaka hiyo kwa haraka ili huduma iendelee kwa ajili ya upatikanaji wa maji.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuitembelea Kata ya Kihurio na Kata ya Bendera na kujaribu kutatua matatizo. Mheshimiwa Waziri, nikwambie kwamba umetatua matatizo ya Kata ya Bendera, lakini matatizo ya maji kwa Kata ya Kihurio yamezidi kuwa mabaya zaidi na sasa wananchi wengine wamekuwa wakidanganywa na kupewa maneno ya kuichafua Serikali na kumchafua Mbunge: -

Je, Waziri utaniambia nini kuhusu maji Kata ya Kihurio ninapotoka mimi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge. Kwa kweli nimefika katika jimbo lake na tumekwenda katika kata inaitwa Bendera, hapakuwa na mradi wa maji kabisa na tulitoa maelekezo na sasa watu wanapata maji pale Bendera. Huu ni utatuzi na Mheshimiwa Mama Anne Malecela, wewe ni mkombozi hasa katika eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo la Kihurio, nitoe maelekezo ya haraka kwa Meneja wa RUWASA wa mkoa na timu yake, hivi tunavyozungumza kesho wawe Kihurio, nami Mheshimiwa Mbunge naomba tukae tuzungumze kwa pamoja ili tuoneshe msukumo wa pamoja kukamilisha mradi huu na wananchi waweze kupata maji.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Pia namshukuru Mheshimiwa Waziri na Wizara yake kwa namna anavyopambana na changamoto inayoendelea Nkasi.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa inayotukumba kama Taifa ni kwa sababu ya miradi tunayoitumia ni mabwawa ambayo yanategemea kupata mvua. Inapotokea mabadiliko ya hali hewa, ndiyo changamoto inaonekana kama hivi sasa.

Je, Serikali ni lini mtaanza kutumia Maziwa makuu badala ya hivi ilivyo sasa inapotokea mabadiliko tunapata changamoto? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Mbunge. Ni kweli sisi Wizara yetu ya Maji Mheshimiwa Rais alishatupatia maelekezo mahususi kwamba yeye ni mama, hataki kusikia wamama wa nchi hii wakiteseka juu ya adha ya maji. Wizara ya Maji itumie rasilimali toshelevu na yeye yupo tayari kutoa fedha kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wanapata huduma ya maji safi na salama. Kwa hiyo, ndiyo uwelekeo wa Serikali hii ya Mheshimiwa Rais Samia Hassan kutumia rasilimali toshelevu hususan maziwa na mito mikubwa ili kuhakikisha wananchi wanapata maji safi.

Mheshimiwa Spika, kwa Mkoa wa Rukwa, Ziwa Tanganyika ndiyo mkombozi kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto ya maji. Ahsante sana.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Sengerema kuna mradi wa maji ambao unasubiri kuwekwa kwenye tangazo kwa ajili ya tender. Hili jambo limechukuwa muda mrefu sana. Sijui Waziri anasemaje mradi wa Kata ya Mabiru, katika Kata ya Igalula? Ni mradi wa siku nyingi.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, miradi ya maji pamoja na ujenzi wake unakuwa na taratibu zake, hasa katika eneo la manunuzi. Nataka nimhakikishie, tunakamilisha hizi taratibu, lakini huu ni mradi mkubwa na nimhakikishie, saini yake nitaishuhudia mimi mwenyewe pale Sengerema. Ahsante sana.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, maswali yangu mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza: Mchakato wa ununuzi wa mabomba ambao ulikuwa unasimamiwa na Wizara na baadaye kurudishwa mkoani, sasa ni lini Serikali itaharakisha mchakato huo wa manunuzi ili wakazi wa Busangi waweze kutumia maji katika eneo hilo?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili: Mkandarasi anayejenga mradi unaotoka Mangu – Ilogi bado ameendelea kuchelewesha malipo ya wafanyakazi: Ni lini Serikali itamhimiza mkandarasi huyo ili aweze kuwalipa watumishi wake fedha hizo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maji imeangalia namna ya kutatua tatizo la maji hasa maeneo ya vijijini. Tumeanzisha Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) na Bunge lako Tukufu tunalishukuru. Tunapoanzisha taasisi yoyote tunakuwa na mikakati. Tumeweka kwa ajili ya manunuzi wizarani, sasa yameshuka mikoani. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wizara yetu itaendelea kufanya marekebisho ili kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya maji inafanyika kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, malipo ambayo mkandarasi amekuwa akichelewesha kulipa watumishi wanaofanya kazi, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kwa kuwa baadaye saa 7.00 Bunge litakuwa limeasitishwa, tukutane ili tuzungumze na Mkandarasi moja kwa moja kwa ajili ya malipo ya watumishi wake. Ahsante sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tarehe 6/6/2022 Serikali yetu iliingia mkataba wa ujenzi wa mradi wa maji kutoka Mto Ruvuma kuja Mji wa Mangaka, miezi minne imefika. Naomba kupata kauli ya Serikali, ni lini mkandarasi atakuwa site ili kutekeleza mradi huo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kweli eneo la Nanyumbu ni eneo ambalo limekuwa na changamoto sana ya maji. Tumesaini mradi huu tarehe 6/6/2022 kama alivyoeleza, kwa sasa tuna-process advance payment kwa Mkandarasi ili kuhakikisha kwamba anakwenda kutekeleza mradi kwa haraka na wananchi wake waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali ilikubali kutoa Shilingi milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa tenki la kuchujia maji: Je, ni lini pesa hiyo itatolewa ili ujenzi huo uanze?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ni kweli tulitoa ahadi na ahadi ni deni. Nimwahidi Mheshimiwa Mbunge ndani ya mwezi huu tutaoa pesa kwa sababu tumeshapokea pesa za Mfuko wa Maji na tutawapa kipaumbele katika Jimbo lake.
MHE. DANIEL T. AWACK: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nishukuru Serikali kwa bei elekezi katika eneo la Mji wa Karatu. Pamoja na shukrani hizi nina swali moja la nyongeza. Je, ni lini Serikali itatoa bei elekezi katika maeneo mbalimbali vijijini kutokana na kwamba kwa sasa bei ni tofauti kati ya kijiji na kijiji na hizi bei huwa inaamuliwa na Jumuiya za Maji Vijijini? Je, ni lini Wizara itatoa bei elekezi katika maeneo mbalimbali katika Jimbo la Karatu?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, kubwa ambalo nataka nilieleze Wizara yetu ya Maji eneo la vijijini, tunatoa huduma kupitia Taasisi yetu ya Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA). Tulifanya tathmini kuona baadhi ya maeneo ya mjini na vijijini unakuta eneo la vijijini walikuwa wakilipa gharama kubwa katika suala zima la ulipaji wa maji. Wizara imeshatoa bei elekezi, ipo miradi ambayo inatumia nishati ya umeme, ipo miradi ambayo inatumia nishati ya jua. Kwa hiyo tumetoa maelekezo kila mradi kutokana na pump zinazotumika imewekwa hela yake rasmi kwa ajili ya kulipa hususan kwa maeneo ya vijijini.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itapeleka miradi ya maji katika Vijiji vya Lusawa, Mdoha, Ukuba na Janda katika Jimbo la Buhigwe?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali ina mpango gani wa kutumia maji ya Mto Malagarasi kutatua changamoto ya maji katika Mkoa wa Kigoma? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais, mkakati wa Wizara yetu ya Maji hasa maeneo ya vijijini kuhakikisha kwamba itakapofika 2025 asilimia 85 ya upatikanaji wa maji iweze kutekelezeka. Tumeshapokea mitambo 25 na kila mkoa utakuwa na mtambo wake. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge maeneo yale ambayo ameyaainisha tutawapa kipaumbele ili kuhakikisha kwamba tunajenga miradi hii kwa wakati na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, Mheshimiwa Rais ametupa maelekezo mahususi Wizara yetu ya Maji kwamba tutumie rasilimali toshelevu ikiwemo mito pamoja na maziwa ili kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto kwa eneo kubwa sana. Kwa hiyo kikubwa nimhakikishie Wizara yetu ya Maji kwa eneo la Kigoma tumelenga kutumia Ziwa Tanganyika na Mto Malagarasi ili kuhakikisha kwamba tunakwenda kutatua changamoto hii ya maji.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Mradi wa Igongwi ambao unahudumia Kata tatu Matola, Luponde na Uwemba tunashukuru Serikali kwa pale tulipofikia, lakini unasuasua sana. Mheshimiwa Waziri anatoa kauli gani kwa wananchi wa Njombe kuhusiana na mradi huo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, natambua mradi ule ni wa kimkakati ambao utatoa huduma kwa watu wengi sana. Mwezi huu tumekwishapokea zile fedha na moja ya maeneo ambayo tunatakiwa tulipe ni mradi ule. Nataka nimhakikishie mwezi huu tutalipa mradi ule wa maji.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishukuru Serikali kwa majibu hayo na naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu mradi huu ndio utakuwa mkombozi kwa ukanda wote wa Pwani wa Wilaya ya Mkinga. Je, Serikali inataka kutuambia ni lini hasa mradi huu utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kwa kuwa Waziri anaahidi hapa kwamba mradi huu sasa unaenda kuanza, yupo tayari kuandamana nami twende tukafanye mikutano ya kuwaaminisha wananchi hawa kwamba tatizo lao sasa linaenda kuondoka?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Dunstan Luka Kitandula, kwa kweli hali ya upatikanaji wa maji Mkinga yalikuwa ni changamoto kubwa sana na tumefanya jitihada kama Serikali ya kuchimba visima lakini kwa jiografia ile imekuwa ni changamoto.

Kwa hiyo, maelekezo ambayo tumepata na support ya Mheshimiwa Rais ni kuyatoa maji sasa ya Mto Zigi, Tanga na kuhakikisha tunakwenda kutatua tatizo la maji katika Jimbo la Mkinga. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara ya Maji tumetoa maelekezo itakapofika Juni mkandarasi awepo site kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huu mkubwa na historia itakumbuka wananchi wa Mkinga kwa jitihada unazozifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini juu ya kuambatana naye, mimi niko tayari kuongozana naye katika kuhakikisha tunaenda kufanya mikutano ili tuweze kuwahabarisha wananchi juu ya utekelezaji wa mradi huu mkubwa katika Jimbo la Mkinga. (Makofi)
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, changamoto ya maji katika Jimbo la Ushetu ni kubwa sana, lakini pia hata miradi iliyoanzishwa toka mwaka 2019 hasa katika Kata za Saba Sabini, Mkunze na Chambo haijakamilika.

Je, ni lini Serikali itaweza kukamilisha miradi hii ili wananchi hawa wa Ushetu waweze kupata maji safi na salama?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze kaka yangu Cherehani kwa kweli ameingia muda mfupi, lakini amekuwa anawapigania watu wake na si mara moja ameshafika ofisini. Kubwa utekelezaji wa miradi ya maji inategemeana na fedha, tutatoa fedha kwa Jimbo la Ushetu kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati na wananchi wa Ushetu waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mkakati wa Serikali ni kuhakikisha tunatumia sasa maji ya Ziwa Victoria kuhakikisha wananchi wa Ushetu wanaenda kupata maji ya uhakika. (Makofi)
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, tunamshukuru sana Waziri kwamba tumepata mradi wa maji katika Kata ya Mabogini. Lakini baada ya manunuzi ya vifaa havijatosha kufikisha maji Umasaini eneo la Remiti. Je, Serikali ina mpango gani wa kutusaidia?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya, lakini kikubwa nataka nimhakikishie maeneo yote ambayo panaishi watu na wanahitaji maji Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan imetoa maelekezo kuhakikisha tunawafikishia maji na wananchi waweze kupata huduma hii muhimu sana ya maji.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa miji 28 ulikuwa ni mradi mkombozi sana kwenye majimbo ambayo hatujawahi kuona maji ya bomba, kila nikiuliza mnaahidi mwezi mmoja unaniambia nini ili wananchi wangu wapate faraja ya maji ya miji 28?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, lakini nataka nimtie moyo ukiona giza linatanda ujue kumekucha. Taratibu zote zinazohusiana na manunuzi ya mradi wa miji 28 zimekwishakamilika na kabla ya Bunge la Bajeti ya Wizara yetu ya Maji tutakaa na Waheshimiwa Wabunge tukubaliane lini tunakwenda kusaini mradi ule taratibu zote tumeshakamilisha tunaenda kwenye signing ya mradi, ahsante sana.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukipata ahadi ya Serikali kupitia Waziri Aweso kuanza kwa mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria kutoka Busega, Bariadi, Itilima, Maswa na Meatu. Lakini mpaka sasa haujaanza na tuliahidiwa kwamba ungeanza mwezi wa nane mwaka jana. Nini commitment ya Serikali juu ya mradi huu kuanza kwa ajili ya kunufaisha wananchi wote hao niliowataja?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, nikiri maelekezo ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ni kutumia rasilimali toshelevu ikiwemo mito pamoja na maziwa kuhakikisha kuwa tunatatua matatizo ya maji. Tumepata fedha zaidi ya shilingi bilioni 400 kwa ajili ya kutumia Ziwa Victoria na kutatua tatizo la maji katika Mkoa wa Simiyu ikiwemo Bariadi, Busega na Itilima.

Kwa hiyo, mkakati wa Serikali sasa hivi tupo hatua ya kumpata mkandarasi na tupo hatua za mwisho. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mkandarasi atapatikana kwa wakati na utekelezaji wake tunaenda kuanza mara moja. (Makofi)
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kuniruhusu niulize swali moja la nyongeza.

Je, lini Serikali itakamilisha miradi ya maji kutoka Ziwa Victoria katika vijiji vya Mogwe, Ikongolo, Majengo, Kiwembe, Mbiti na Muswa?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge pamoja na Makamu Mwenyekiti wangu wa Kamati, Serikali imefanya jitihada kubwa ya kuyatoa maji katika Ziwa Victoria na kuyaleta katika Mji wa Tabora, Igunga na Nzega. Kazi iliyobaki ni kufanya tu usambazaji.

Nataka nimhakikishie usambazi huo tutaufanya katika vijiji ambavyo amevitaja ili katika kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma ya maji safi na salama.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa wananchi wa Kata ya Isanga na Guduwe Wilaya ya Bariadi wana shida sana ya maji, muda mwingi wakina mama wanaupoteza kutafuta maji kuliko kufanya kazi za maendeleo. Ni lini Serikali itachimba visima virefu katika kata hizo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kwanza kilio cha Wanabariadi kwa maana ya Mkoa wa Simiyu kimesikika na tumepata fedha kama nilivyoeleza zaidi ya shilingi bilioni 400 katika kuhakikisha tunaenda kutekeleza mradi mkubwa. Tumefanya jitihada kubwa za kuchimba visima eneo la Mkoa wa Simiyu, lakini imekuwa ni changamoto. Kwa hiyo, solution pekee kwa ajili ya kutatua tatizo la maji Bariadi na Mkoa wa Simiyu ni kuhakikisha tunayatoa maji ya Ziwa Victoria katika kuhakikisha Wanasimiyu na Wanabariadi wanapata maji safi na salama.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, mradi wa Mhangu - Ilogi ni mradi uliochukua muda mrefu sana na mwaka jana niliuliza swali la msingi na Mheshimiwa Waziri alinipa majibu kwamba mwezi wa sita mwaka jana mradi ule ungezinduliwa. Sasa nataka kufahamu majibu ya ukweli ni lini sasa mradi huo wa Mhangu - Ilogi utakamilika?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ukimwona mtu mzima analia ujue kuna jambo. (Makofi/Kicheko)

Nimwombe Mheshimiwa Mbunge baada ya kipindi cha maswali baada ya saa saba tukutane ofisini ili kuhakikisha kwamba hili jambo tunalikamilisha na wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri umekuwa ukiulizwa maswali ya uhitaji wa maji na Wabunge, na umekuwa ukiwapa wote ahadi za matumaini, lakini tunajua bajeti yako ni ndogo.

Sasa hudhani ni wakati sahihi wa kuliambia Bunge hili tukufu kipi kipaumbele cha Serikali kwa mwaka huu wa fedha? Kwa sababu haiwezekani kila Mbunge amesimama unampa matumaini, lakini matumaini hayatekelezwi.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima uliza swali lako.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nini kipaumbele cha Serikali vijijini, mijini; maeneo gani na kwa mawanda yapi? Kuliko kupeana ahadi hapa unaanza kuulizwa tunataka utupe ahadi ya mwisho, siyo jambo jema.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimtoe hofu, wali wa kushiba unaonekana kwenye sahani. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan imejipanga juu ya kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe mfano, eneo la vijijini kupitia bajeti yetu tunakwenda kutekeleza miradi 1,176 vijijini, haijawahi kutokea. Lakini pia dhamira ya Mheshimiwa Rais sasa hivi katika dola milioni 500 ambazo tumezipata, katika miji 28 tunakwenda kutatua tatizo hili la maji. Kwa hiyo, kipaumbele cha Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha wananchi wa mijini na vijijini wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, naomba kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na miradi mingi sana ya maji ndani ya jimbo letu na tumekuwa tukikuomba uje uikague miradi hiyo kuona ubora wake na thamani ya fedha inayotumika.

Je, ni lini sasa Mheshimiwa Waziri na timu yako utapata nafasi ya kuja kukagua miradi hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimuahidi Mheshimiwa Gulamali baada ya Bunge letu la Bajeti nitafanya ziara katika jimbo lake katika kuhakikisha tunasimamia na kufuatilia miradi katika Jimbo lake la Manonga. Ahsante sana.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Tukuyu una changamoto kubwa sana ya maji ikiwa ni Kata za Bulyaga, Msasani, Bagamoyo, Makandana, Ibigi, Kawetele; na Serikali iliahidi kupeleka shilingi bilioni 4.5 lakini mpaka sasa wamepeleka shilingi milioni 700 tu. Wananchi wa kule hasa akina mama wanaacha kufanya kazi kubwa za kutafuta riziki kwa ajili ya watoto wanashinda kutafuta maji.

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha hizo ili kumalizia mradi huo wa maji? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua maji hayana mbadala, maji ni uhai na Serikali ya Awamu ya Sita ya Mama Samia Suluhu Hassan kila mwezi tunapokea zaidi ya shilingi bilioni 14, 15 katika Mfuko wetu wa Maji.

Nataka nimhakikishie tutawapa kipaumbele Wanatukuyu ili kuhakikisha miradi yake nayo inapata fedha ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati wananchi wapate huduma ya maji.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, mimi nina swali moja tu; kuna upotevu mkubwa sana wa maji Mkoa wa Dar es Salaam hasa kwenye Jimbo la Temeke, nadhani mabomba yale ni chakavu na ya siku nyingi.

Je, mna mkakati gani sasa wa kubadilisha yale mabomba kuweka mabomba mapya ili tusipate taabu ya maji tena?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Temeke kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Ni kweli moja ya changamoto kubwa juu ya miradi ni upotevu wa maji na tumetoa maelekezo mahususi juu ya kuhakikisha kwamba tunakarabati na kujenga miundombinu mipya ili kuhakikisha upotevu huu unakuwa katika standard.

Kwa hiyo, nataka nimhakikishie na kazi kubwa na nzuri inayofanywa na DAWASA katika kuhakikisha tunakarabati na kujenga miundombinu mipya ili upotevu huu usiendelee na wananchi wahakikishe wanapata huduma ya maji safi na salama.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, kwanza naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa ahadi ya kufanya upembuzi yakinifu kwenye mwaka huu wa fedha, lakini Bwawa la Kasamwa pamoja na kuhudumia wananchi limesababisha Kiwanda cha Pamba cha Kasamwa pamoja na Kiwanda cha Mafuta kutofanya kazi kwa sababu hakuna maji. Sasa ni lini baada ya upembuzi yakinifu ujenzi wa bwawa hilo utafanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nawapongeza GEUWASA, wanafanya kazi yao ya kusambaza maji vizuri. Lakini maji ya GEUWASA ni ya nyumbani (domestic) na maji ya bwawa yanategemewa kwa ajili ya mifugo na kuna mnada mkubwa pale wa mifugo. Sasa ni lini ujenzi wa bwawa hilo utapewa kipaumbele ili kuokoa mifugo inayokwenda Kasamwa pale? Nakushukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimtoe hofu Mheshimiwa Constantine Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kwa kazi nzuri anayoifanya, lakini nataka nimhakikishie kuwa kupitia Wizara yetu ya Maji tumepata fedha kwa ajili ya kununua mitambo seti tano kwa ajili ya uchimbaji wa mabwawa. Kwa hiyo, moja ya maeneo ambayo tutaweza kuwapa kipaumbele ni eneo katika Jimbo lake la Geita Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kikubwa, nataka nimhakikishie kuwa mitambo itakapokuwa imefika mwezi huu wa Juni, moja ya maeneo ambayo tutayapa kipaumbele ni eneo la Geita kwa sababu kumekuwa na uhitaji mkubwa sana. Ahsante sana.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itasafisha ili kuongeza kina cha Bwawa la Lukuledi ikiwa ni ahadi yake Mheshimiwa Waziri ya mwaka 2021, maji ambayo yanatumika katika Vijiji vya Lukuledi, Mwangawaleo, Ndomoni, Mraushi na Nambawala?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa moja ya changamoto kubwa katika utekelezaji wa mabwawa ilikuwa suala zima la vifaa. Lakini tumekwishapata fedha juu ya ununuzi wa vifaa hivi vya kisasa na moja ya maeneo ambayo tutayapa nguvu na ya kipaumbele ni kuhakikisha kwamba tunajenga mabwawa. Kwa hiyo, tutawapa kipaumbele katika kuhakikisha mabwawa ambayo yatakayokuwa yamejengwa na yeye jimboni kwake.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Mwanza tumekuwa na shida sana na kero ya maji, na hasa miradi ambayo haitekelezeki, na ukizingatia Mwanza tumezungukwa na ziwa.

Je, ni lini Serikali itatekeleza miradi ya maji katika Mkoa wa Mwanza tukaondokana na kero ambayo inatukumba mpaka muda huu?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri katika Jiji la Mwanza pamoja na mradi tuliokuwa nao lakini ongezeko la watu limesababisha uhitaji mkubwa wa maji. Tuna mradi sasa hivi tunaongeza chanzo katika eneo la Butimba ili kuongeza uzalishaji na wananchi hawa waweze kupata huduma ya maji safi na salama. Tumepata fedha zaidi ya shilingi bilioni 65 katika kuhakikisha kazi ile inaanza na mkandarasi yuko site.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa sisi kama Wizara ya Maji tutausimamia na kuufuatilia mradi ule ukakamilike kwa wakati ili uweze kuongeza uzalishaji na wananchi wa Jiji la Mwanza kwa maana ya Ilemela pamoja na Nyamagana kuweza kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi na kwanza nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri ambaye wakati alipokuwa jimboni kwangu mara ya mwisho alitoa maelekezo ya namna ya kutatua changamoto ya mafuriko yanayosababishwa na kufukiwa korongo la Mto Nduruma na kutesa wananchi wa Kata za Shambarai Burka, Mbuguni, Majengo na Makiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya ziara ya wale wataalam ambao walitumwa...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Pallangyo swali.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: ...kimya kimetanda. Swali sasa, je, Serikali ina mkakati gani wa kutenga fedha kwa ajili ya kwenda kutatua ile changamoto ya mafuriko?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nimefanya ziara katika Jimbo la Mheshimiwa Mbunge la Arumeru Mashariki na moja ya ahadi ni kuwapatia fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshatoa fedha mwezi huu, shilingi milioni 100, kwa ajili ya uanzaji wa kazi ile. Mheshimiwa Mbunge unaweza ukafuatilia katika hilo. (Makofi)
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na ahsante kwa Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali.

Je, Mheshimiwa Waziri unatuhakikishia pamoja na usanifu huo wa kutoa maji Ziwa Tanganyika kuleta katika Mkoa wetu wa Katavi. Je, usanifu huo utaambatana pamoja na ufungaji wa mita za uhakika ambazo zitaenda kuondoa tatizo la ubambikizwaji wa bili kwa wananchi wa Mkoa wa Katavi? Ahsante.(Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge Dada yangu Martha kwa kazi kubwa anayoifanya katika Mkoa wa Katavi, kwa kweli ni kielelezo chema kwa ajili ya kuwapigania wananchi wa Katavi kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie kwamba tumepewa maelekezo mahsusi na Mheshimiwa Rais kuhakikisha tunatumia rasilimali toshelevu kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. Nimhakikishie kwamba tunapokwenda katika bajeti hii 2022/2023 na asubiri katika bajeti yetu ya Wizara yetu ya Maji tumejipanga katika kuhakikisha tunakwenda kutumia chanzo cha Ziwa Tanganyika ili wananchi wa Katavi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, pili ni juu ya suala zima la malalamiko ya bili za maji. Wizara ya Maji tumeendelea kufanya mageuzi makubwa sana na hata katika wiki yetu ya maji tumeshaanza kuweka mifumo katika kudhibiti, pia katika kuhakikisha tunamaliza tatizo hili la maji kabisa la bili, tumeona kabisa kizuri huigwa tunaona sasa ni muda wa kutumia teknolojia zilizopo kwa kuanzisha prepaid meter kwa maana ya mita za maji (LUKU) ili kuhakikisha kwamba tunaondokana na tatizo la hili la maji.

Mheshimiwa Spika, tumesharuhusu wadau mbalimbali wameshaweza kufunga ili kuweza ku-study na muda si mrefu tutatoa maelekezo kwa ajili ya uanzaji wa hizo mita za maji(LUKU). Ahsante sana.(Makofi)
MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Je, Serikali itakuja lini na mpango wa kusambaza maji katika vijiji vya Wilaya za Mkoa wa Mara zinazozunguka Ziwa Victoria ukizingatia tayari vyanzo vya maji viko wazi kutokana na Ziwa Victoria na vijiji vingi havina maji? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Dada yangu Agnes Marwa na atakubaliana na mimi Wizara ya Maji tumewekeza miradi mikubwa sana katika Mkoa wa Mara. Tuna mradi wa Mugangu, Kyabakari Butiama, zaidi ya Bilioni 70. Pia tuna mradi pale Bunda ambao umekwishakamilika kwa ajili ya chanzo.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie kila ambapo bomba kuu litakapokuwa linapita vijiji jirani tutahakikisha vinapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. KABULA E. SHITOBELO: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi napenda niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati miundombinu ya maji katika Jimbo la Kwimba, Misungwi, Ilemela, Sengerema na Nyamagana?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Serikali imeendelea kujitahidi na inaendelea kuwekeza kuhakikisha kwamba tunakarabati na kujenga miundombinu mipya kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama. Mathalani kwa eneo la Misungwi tumeshakwenda na Mheshimiwa Rais na tumekwishazindua mradi mkubwa wa zaidi ya Bilioni 12 katika kuhakikisha wananchi wale wanapata huduma ya maji safi na salama, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. THEA M. NTALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami napenda kuuliza Lake Nyasa ina maji ya kutosha sana. Serikali ina mpango gani wa kutumia yale maji angalau vijiji vile karibu na lake vipate maji ya kutosha? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na pia nikubaliane nae. Sisi kama nchi hapa palipofikia hatuna sababu tena ya kulalamika juu ya changamoto ya maji, lazima tukubali tutumie rasilimali toshelevu tulizonazo ambazo Mwenyezi Mungu ametujalia katika kuhakikisha tunawekeza miradi mikubwa na kutatua matatizo ya maji.

Mheshimiwa Spika, tumeona jitihada za Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan juu ya uwekezaji wa miradi mikubwa tunataka kuyatoa maji ya Ziwa Victoria kuyaleta Dodoma. Pia mpango wetu ni kuhakikisha maji ya Ziwa Tanganyika yanaenda kuwanufaisha wananchi katika eneo hilo la Mkoa wa Ruvuma. (Makofi)
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Serikali inayo mpango wa kuleta maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria hapa Dodoma lakini ambako Ziwa Victoria lipo katika Mkoa wa Mwanza kwenye Jimbo la Sumve hakuna maji ya uhakika ya bomba kutoka Ziwa Victoria. Serikali imekuwa ikiahidi kwamba itatupelekea maji hayo kwa bajeti mbili mfululiozo.

Je, ni lini sasa Serikali itapeleka maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria katika Jimbo la Sumve?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na nimwambie tu kwamba baada ya dhiki sio dhiki, baada ya dhiki ni faraja. Jitihada kubwa zimefanyika katika Mkoa wa Mwanza Majimbo yote yamefikiwa na uwekezaji wa mradi wa Ziwa Victoria kasoro Jimbo la Sumve.

Mheshimiwa Spika, ni muda muafaka sasa katika bajeti yetu hii tunayokwenda nayo 2022/2023 kuhakikisha tunapeleka sasa maji ya Ziwa Victoria katika Jimbo lako la Sumve.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto kubwa ya maji inayotukumba katika Mkoa wetu wa Mtwara hususan kwenye Jimbo langu la Mtwara Vijijini. Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia chanzo cha maji cha Mto Ruvuma?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nataka niweke bayana rasilimali za maji tulizonazo juu ya ardhi na chini ya ardhi ni zaidi ya Bilioni 126. Bilioni 105 ni maji yaliyopo juu ya ardhi, kikubwa ni lazima rasilimali hizi toshelevu tulizonazo zitumike. Kwa eneo la Mto Ruvuma kwa maana ya Mtwara
tukitumia chanzo cha Mto Ruvuma tutamaliza kabisa tatizo la maji katika Mkoa wa Mtwara. Kwa hiyo, hiyo ni dhamira yetu na Serikali tuna maongezi na wadau mbalimbali naamini imani hii tunakwenda kuitekeleza na kuhakikisha wananchi wa Mtwara wanaenda kuondokanana tatizo kabisa la maji. (Makofi)
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba nifahamu ni lini Serikali itakamilisha usambazi wa maji Ziwa Basutu ambako imefikia tu eneo moja kwa sasa na maeneo yaliyotarajiwa ni 12?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge, kwanza anafanya kazi kubwa nzuri na nimekwishafika katika Jimbo lake. Kikubwa ahadi ni deni, Serikali na dhamira ya Rais wetu tutahakikisha kwamba tunakwenda kuyatumia maji yale ya Ziwa Basutu na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Kwa kuwa, Serikali imewekeza sana katika hii miradi ya maji vijijini na changamoto ninayoiona katika vile Vyama vya Ushirika vya maji ni kukosa mfumo mzuri wa kukusanya mapato. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia kupata drilling system itakayosadia kukusanya maji kiurahisi?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza ninathamini mchango mkubwa na jitihada kubwa za uwekezaji wa miradi ya maji vijijini. Serikali kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini katika kuhakikisha inatatua tatizo la maji vijijini. Tumeona tuna jumuiya zetu hizi za watumiaji maji, changamoto kubwa jumuiya za watumiaji maji ni katika suala zima la usimamizi. Moja tumetoa maelekezo kwamba katika kila mradi sasa kutakuwepo na Technician kupitia wananfunzi ambao wanatoka katika Chuo cha Maji. Pili, tunataka kila mradi lazima awepo Mhasibu ambaye ataweza kusimamia na kuhakikisha kwamba tunaweka mifumo.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tutatangaza mfumo rasmi wa kuhakikisha kwamba wanakuwa na bei rahisi hata vijijini ili katika kuhakikisha wanapata huduma ya maji bila ya usumbufu wowote.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi.

Je, ni lini Serikali itatumia chanzo cha Ziwa Rukwa kulisambazia Jimbo la Momba maji ili kuondoa kadhia na changamoto ya maji ambayo tunaipata?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Kwa kweli vyanzo toshelevu ndiyo suluhu ya matatizo ya changamoto katika Majimbo mbalimbali. Kwa hiyo, mkakati wa Wizara na maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha kwamba tunatumia rasilimali toshelevu katika kuhakikisha kwamba tunatatua matatizo ya maji.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunajitahidi kutafuta fedha katika kuhakikisha kwamba tunatumia rasilimali toshelevu na wananchi wako wa Momba hatutowasahau katika kuhakikisha tunatatua tatizo la maji. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami niulize maswali mawili ya nyongeza. Nkasi hatuna shida na uwajibikaji wako Mheshimiwa Waziri, changamoto ni kwamba kwa kuwa umetambua kwamba tuna Ziwa Tanganyika lakini bado hatuna maji kwa hiyo hatuna shida na chanzo. Ni lini utaonyesha uthubutu kuepusha fedha ambazo zinatumika kwenye usanifu na bado miradi haijakamilika lini utakamilisha huo mradi wa maji ili na sisi watu wa Nkasi tuweze kupata maji ya uhakika?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili kwa kuwa Mheshimiwa Waziri mwenyewe alifika Nkasi mwaka jana na akatoa fedha, ukawaambia kwamba mwezi Desemba mradi huo utakamilika wa maji lakini mpaka leo nazungumza hizo Kata Tano za pale Mjini hazina maji. Ni lini sasa mtaachana na hizi fikra za kutumia visima badala ya kuelekeza nguvu zote ili kusaidia sasa Mkoa mzima badala ya Wilaya ya Nkasi peke yake? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Aida, kwa kweli nimefika Nkasi na unafanya kazi kubwa unafanya kazi nzuri. Kubwa Mwenyezi Mungu hawezi kukupa fursa ya Ziwa halafu akakupa fursa ya kuchimba visima. Maeneo mengi ambayo yamekuwa na Maziwa mengi ukichimba visima tunafeli. Kwa hiyo, namna pekee ya kuhakikisha tunatatua tatizo la maji eneo la Rukwa ni kuhakikisha tunatumia Ziwa Tanganyika na kazi hiyo imekwishaanza.

Mheshimiwa Spika, kubwa nimuombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kutupa ushirikiano na Wizara ya Maji hatutomuacha katika Jimbo lake la Nkasi kuhakikisha wananchi wale wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili tulifika katika mradi ule wa Namanyele, Mkandarasi alikuwa anadai kiasi cha fedha na fedha tumeshampa sasa wananchi wanapata huduma ya maji. Kikubwa ni kuongeza sasa usambazaji ili wananchi wa eneo lile waendelee kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tuko tayari na tutashirikiana bega kwa bega katika kuhakikisha wananchi wake katika eneo la Namanyele wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri Mkoa wa Mbeya una vyanzo vingi sana vya maji lakini chanzo kikubwa tunaliona Ziwa Nyasa ni kama linaweza likatatua tatizo la maji.

Ni lini Serikali mtaweka fedha pale ili Wilaya zote Saba ziweze kupata maji kwa kupitia Ziwa Nyasa? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mbunge nikushukuru sana. Tunatambua kabisa katika eneo la Mbeya kumekuwa na ongezeko kubwa pamoja na uwekezaji wa miradi ya maji. Tumepata ombi maalum la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini...

SPIKA: Mheshimiwa Waziri mbona hapo kama umepunguza sauti au mimi ndiyo sijakusikia. (Kicheko)

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nirudie kwamba tumepata ombi maalum la Mheshimiwa Mbunge wa Jiji la Mbeya Mheshimiwa Spika kwamba tukitumia chanzo cha Mto Kiwira tunakwenda kumaliza kabisa tatizo la maji. Kazi hiyo tumeshapata Mhandisi Mshauri na tumeshasaini mkataba Mheshimiwa Spika nataka nikuhakikishie sisi ni Wizara ya Maji si Wizara ya Ukame. Tutahakikisha ndoto ile ambayo umeilenga tunaenda kuitekeleza na wananchi wa Jiji la Mbeya wapate huduma ya maji safi na salama. (Makofi)
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami kunipa nafasi niulize swali moja kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, katika moja ya safari zake ambazo Mheshimiwa Waziri alifanya Mkoani Rukwa alifika Kalambo na akafika Ziwa Tanganyika eneo la Kasanga na alijionea jinsi ambavyo tuna utajiri mkubwa sana wa maji. Sasa katika majibu yake sijamsikia katika utafiti ambao unaendelea kama na chanzo kile cha kutoka Kasanga nacho ataki-consider ili kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Mkoa wa Rukwa kwa ujumla, Songwe na ikiwezekana hata Mbeya maana maji ni mengi sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kauli ya Mheshimiwa Waziri.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru sana lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge. Kwa kweli nilifanya ziara na akanipa ombi maalum la kwenda kunionesha eneo lile, nikushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, tumefanya ugunduzi mkubwa sana na nimwombe sasa tuwaachie wataalam, lakini bila kuwaachia tu wataalam na sisi tuendelee kutoa mawazo yetu ni namna gani sasa rasilimali ile toshelevu tuliyonayo iende kunufaisha Kalambo na maeneo mbalimbali mengi ili katika kuhakikisha tunatatua matatizo ya maji, ahsante sana.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tatizo hili ambalo liko Nkasi na sawa na tatizo ambalo liko Biharamulo hasa tukitegemea kwamba tuna mradi mkubwa wa kutoa maji Ziwa Victoria kuyaleta katika Mji wa Biharamulo.

Ni nini sasa kauli ya Serikali kuhusu utekelezaji wa mradi huo katika mwaka huu wa fedha? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Engineer Ezra, kwa kazi kazi kubwa nzuri anayoifanya katika Jimbo lake la Biharamulo.

Mheshimiwa Spika, namna ya kutatua tatizo la maji Biharamulo ni kuhakikisha tunaanzisha mradi mkubwa wa kutumia Ziwa Victoria na tumeanza jitihada katika maeneo mbalimbali. Nimwombe awe mvumilivu, nadhani kipindi ambacho tutaisoma bajeti yetu tarehe 12 mambo yatakuwa bambam, tuko pamoja. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mwezi mmoja uliopita nilisoma kwenye vyombo vya Habari kwamba vyombo vya ADB imepitisha zaidi ya bilioni 250 kwa ajili ya Bwawa la Farkwa. Sasa nataka kujua ni lini mradi huo utaanza? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge amekuwa mfuatiliaji mkubwa sana juu ya ujenzi huo wa mradi huo wa Bwawa la Farkwa. Utekelezaji wa miradi ya maji inategemea na fedha na hapa, nitumie nafasi hii kumpongeza sana nakumshukuru Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake mahususi kabisa, African Development Bank bodi yake imeridhia sasa kutupatia fedha ya kuhakikisha ujenzi wa bwawa lile unatekelezeka. Kwa hiyo, suala la mikopo lina taratibu zake, lakini kikubwa tutaliharakisha ili kuhakikisha mradi ule unaenda kuanza na wananchi wa Farukwa kwa maana ya Jimbo lake la Chemba na wananchi wa Jiji la Dodoma waende kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza ninashukuru sana Serikali kwa jitihada ambazo zimeshaanza kufanyika katika ukanda wa Ziwa Nyasa. Kwa kuwa, Jimbo hili lina pande kuu mbili za Umatengo na Ziwa Nyasa, katika eneo hili la Umatengo kuna Kata ya Lumeme Kijiji cha Luhindo, Uhuru na Mipotopoto lakini pia Kata ya Luhangalasi zina tatizo kubwa sana la maji.

Je, Wizara ina mpango gani wa kupeleka fedha za dharura kwa ajili ya kuvisaidia vijiji hivi angalau hata kama ni Shilingi Milioni Moja.

Swali la pili, katika ukanda wa mwambao uliozungumzia kuna Kijiji cha Mtupale na Chiwimbi hivi havijazungumzwa, Je, mpango wa Serikali ni nini ili kuhakikisha na wenyewe wanapata maji? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya, Wizara ya Maji pamoja na mpango mkakati wa kuhakikisha tunatumia rasilimali toshelevu, kwa maana ya mito na maziwa Wizara ya Maji imejipanga sasa hivi tuna mitambo katika kila Mkoa, moja ya maelekezo ambayo niyatoe na tunashirikiana na Mheshimiwa Mbunge eneo hilo ambapo kama kuna tuwezekano wa kupata maji ya kisima basi tutachimba kwa haraka kuhakikisha wananchi wake wanaanza kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa nataka nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, tarehe 10 Mei, bajeti yetu ya Wizara ya Maji tunawasilisha kwa hiyo moja ya mikakati mizuri ambavyo tumejipanga ni kuhakikisha tunakamilisha changamoto ya maji kwa kiwango kikubwa sana. Ahsante sana.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na fedha ya dharura iliyotoka Wizarani kwako Mheshimiwa Waziri, bado haijamaliza changamoto ya maji Jimbo la Nkasi Kaskazini. Tunapenda kufahamu mchakato wa kutoa maji Ziwa Tanganyika kusambaza kwenye Mkoa wa Rukwa umefikia wapi?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu Mwenyezi Mungu ameijalia tuna rasilimali za maji juu ya ardhi na chini ya ardhi mita za ujazo bilioni 126, maji yaliyokuwa juu ya ardhi ni zaidi ya mita za ujazo bilioni 105. Maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha tunatumia rasilimali hizi toshelevu kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mpango mkakati wa Wizara yetu ya Maji na tutawasilisha katika bajeti yetu ya Terehe Kumi Mwezi wa Tano ni kuhakikisha tunatumia Ziwa Tanganyika kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji Kigoma, Mkoa wa Rukwa na Mkoa wa Katavi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, kuna baadhi ya vitongoji katika vijiji hivyo havijawekwa kwenye orodha ya mpango wa kuwekewa vitu kwa ajili ya kuchotea maji. Je, Serikali inaweza kupokea maombi mapya sasa maalum kwa ajili ya kuongeza vituo vya kuchotea maji kwenye vijiji ambavyo vimepitiwa na mradi huu?

Swali la pili, miradi mingi kwenye Halmashauri zetu imekwama kwa sababu ya upatikanaji wa mabomba ambayo yananunuliwa kwa pamoja kupitia RUWASA Makao Makuu.

Je, Serikali sasa inatuhakikishiaje kwamba mabomba sasa yanakwenda kupatikana kwa wakati ili kutokukwamisha miradi mingi kwenye Halmashauri zetu?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya jukumu mahsusi na Wizara ya Maji ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama, tunao huu mradi mkubwa ambao unajengwa na kuna baadhi ya vitongoji ameviainisha ambavyo vinahitaji maji, nataka nimhakikishie kukamilika kwa mradi huu na hivyo vitongoji navyo vitapokea kuhakikisha nao wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji kupitia Wakala wa Maji Vijijini ni kuhakikisha tunatatua changamoto ya maji katika maeneo ya vijijini. Tulikuwa na changamoto ya manunuzi na tumepewa ombi na maelekezo ya Bunge ni kuhakikisha manunuzi haya yanafanyika katika maeneo ya Mikoa, tulishakaa na wenzetu wa manunuzi kwa maana ya RUWASA maelekezo ya Wizara ni kwamba manunuzi yote yanatakiwa kufanyika katika Mikoa husika ili kuharakisha utekelezaji wa miradi. (Makofi)
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mnamo mwaka 2021 Mheshimiwa Waziri Mkuu aliweka Jiwe la Msingi wa ujenzi wa mradi wa maji katika Kijiji cha Kifura ambao wakati huo ulikuwa asilimia 43, mpaka leo mradi huo umetelekezwa na uko asilimia 43 hiyohiyo. Je, ni nini mpango wa Serikali kutenga fedha ili kukwamua mradi huu wa maji ili wananchi wa Kifura waweze kupata maji?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mbunge, kubwa mradi huu wa Kifura ni mradi ambao ulikuwa unatekelezwa na kampuni ya Nangai pamoja na taasisi ambayo inaitwa ENABEL, tulikuwa na changamoto baina ya huyu Mkandarasi na hii taasisi, tumekwisha kaa nao na moja ya maelekezo ambayo tumempatia yule Mkandarasi, Tarehe 31 Agosti, akabidhi mradi huo ili wananchi wa Kifura waendelee kupata huduma ya maji safi na salama.(Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nianze kuipongeza Serikali ya Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kusambaza maji vijijini. Je, wizara iko tayari kushusha bei ya maji Wilaya ya Nyang’hwale kutoka 1,700 kwa unit na kufanya iwe 1,500 ili kuhamasisha wananchi wengi kuweza kujiunga na mtandao huo wa maji? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni haki ya mwananchi kupata huduma ya maji lakini mwananchi naye asisahau anao wajibu wa kulipia bill za maji. Kwa hiyo, ameonesha hiyo changamoto na nimuombe basi Saa Saba tuweze kukaa na timu yetu tuone namna nzuri ya kuhakikisha wana Nyang’hwale tunatatua changamoto hiyo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naishukuru sana Serikali kwa kutusaidia kuweka miradi ya maji kwenye vijiji takribani Vinne kikiwemo Kijiji cha Matare pale katika Jimbo la Singida Mashariki. Hoja yangu na swali langu Mheshimiwa Waziri, mradi umekamilika na Mkandarasi amemaliza kazi changamoto iko kwenye umeme na tumeshalipia watu wa TANESCO mpaka leo umeme haujawekwa.

Je, ni lini Serikali itahakikisha umeme unawekwa ili wananchi wa Matare waanze kutumia maji. (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Wizara ya Maji inafanya kazi kwa ukaribu sana na Wizara ya Nishati na wamekuwa msaada mkubwa kwetu, hili jambo tutalifuatilia kwa haraka kuhakikisha ujenzi wa eneo hilo linakamilika kwa haraka. Ahsante sana.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Mradi wa Maji Kyerwa, Nyaruzumbula mpaka Kamuli ni lini utaanza?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama nilivyoeleza Tarehe 10 mwezi Mei, tunawasilisha bajeti yetu, nataka nimhakikishie kama Mheshimiwa Rais alivyosema mambo ni moto, mambo ni fire tutakwenda vizuri katika kuhakikisha jambo hili linaenda vizuri. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Waziri mradi wa Nduku - Msangi – Ntobo ni mradi ambao umechukua muda mrefu sana, kwa hatua iliyofikiwa sasa wameweza kukosa kiasi cha Shilingi Milioni 50 tu kwa ajili ya Mkandarasi kuchimba mtaro, kuchelewa kwa mradi huu kumesababisha sasa Hospitalli ya Wilaya ya Ntobo kukosa maji na hivyo kupelekea mlipuko wa magonjwa mbalimbali kwenye hospitali ile ya Wilaya.

Je, ni lini sasa Wizara itatoa kiasi hiki kwa dharura ili ipeleke fedha hizo hospitali ya Wilaya iweze kupatiwa maji?

Swali langu la pili, Kata niliyoitaja hapa kwa maana ya Mwakata imepitiwa na bomba kuu linalotoka Kagongo kwenda Isaka na Kata hii haina maji. Je, ni nini sasa mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba Kata hii na yenyewe inanufaika na maji hayo kwa sababu bomba hilo limepita maeneo hayo? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Kaka yangu wa Msalala kwamba Wizara ya Maji mwezi huu tumepokea Bilioni 67 kwa ajili ya malipo ya Wakandarasi. Kwa hiyo, moja ya maeneo ambayo tutayapa kipaumbele cha haraka ni eneo la Msalala kuhakikisha mradi huu unakamilika na wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni juu ya mradi ambapo bomba kuu linapita. Sera inasema bomba kuu linapopita vijiji ambavyo vipo karibu na kilomita 12 kulia na kushoto mwa bomba kuu, vinahakikishiwa kwamba vinapata huduma. Nataka nimhakikishie hili tumelipokea na tunaenda kulifanya kazi kuhakikisha kwamba Kata hiyo nayo inapata huduma ya maji safi na salama.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mheshimiwa Waziri ulituahidi mwaka jana kwenye Bunge la Bajeti ungetuchimbia visima katika shule za Kata ndani ya Manispaa ya Iringa, ulipokuja kwenye Wizara Rais mwezi wa Agosti uliahidi kuleta gari katika Mkoa wa Iringa ili tuweze kupata huduma hiyo ya visima, sasa hatijachimbiwa visima mpaka leo.

Swali langu ni; kwanza, huogopi kwenda motoni?

Namba Mbili; mnatuchimbia lini visima?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, tuliomba kuwa na magari kwa ajili ya uchimbaji visima katika kila Mkoa, magari yale tumekwishayapata na katika kila Mkoa tumekwishayapeleka. Ninamuomba Mheshimiwa Mbunge katika yale maeneo ambayo anaona tunahitaji uchimbaji visima, kwa sababu vitendea kazi tunavyo, hatuna kisingizio chochote. Kwa hiyo, jukumu letu ni kuhakikisha maeneo ambapo panatakiwa kuchimbiwa visima tunakwenda kuchimba visima. Ahsante sana.
MHE. ASK. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mradi mkubwa wa maji unaotokea Ruvu Chini kukamilika lakini baadhi ya Kata za Jimbo la Kawe kama Mbezi Juu hazina maji kabisa. Nini kauli ya Serikali?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, kubwa mradi ule mkubwa tumeshaukamilisha na Mheshimiwa Waziri Mkuu katika wiki ya maji alikuja kuuzindua, kazi iliyobaki ni suala zima tu la usambazaji. Kwa hiyo, kikubwa tutaongeza kasi juu ya usambazaji maeneo haya ya Mbezi Juu na maeneo mengine kuhakikisha kwamba wanapata huduma ya majisafi na salama.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mkoa wa Tabora ni moja kati ya Mikoa ambayo imenufaika na mradi wa maji ya Ziwa Victoria. Jimbo la Tabora Mjini ni moja kati ya Majimbo hayo ambayo yamepata maji hayo lakini Kata zilizoko pembezoni mpaka sasa hazijanufaika na maji hayo.

Je, Serikali mna mpango gani wa kupeleka fedha ili iwasaidie kusambaza maji na wananchi wetu waweze kunufaika na mradi huo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninamshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuthamini kazi kubwa ambayo imefanywa na Serikali, kulikuwa na mradi mkubwa zaidi ya Bilioni 600 kuyatoa maji Ziwa Victoria kuyapeleka Tabora, Nzega hadi Igunga. Nataka nimhakikishie maeneo hayo yote ya pembezoni ambayo yanahitaji maji tutayafikia kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya majisafi na salama na tutatoa fedha Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri, na especially commitment ya Serikali kwamba Mradi huu wa Maji ya Ziwa Victoria unaanza katika mwaka wa fedha huu wa 2023/2024. Lakini kama ulivyosema, utekelezaji wa miradi ya maji kwa Biharamulo uko asilimia 65 sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, sasa ninaomba, umesema mmetuwekea 2.8 kilometa mtandao. Sasa kwa sababu maji yanakuja, naomba ufanye commitment, kwa sababu sasa bahati nzuri leo najibiwa na Waziri mwenyewe, angalau uniongezee kilometa tatu nyingine waweze kusambaza mabomba zaidi pale mjini ili maji yatakapofika yawafikie wananchi wengi zaidi. Swali la kwanza hilo, naomba tu commitment.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mradi huu wa Maji wa Ziwa Victoria tulikuwa tumeahidiwa pia kutoa maji Ziwa Victoria tupite katika Kata za Nyamigogo, yale Kabindi, Nyabusozi, Nemba yaende Nyantakara yafike mpaka Nyakanazi katika kata ya Lusahunga. Sasa ni lini mradi huu wa kutoa maji za Ziwa Victoria katika line hii ya kuyapeleka mpaka Nyakanazi utatekelezwa na Serikali kwa ajili ya wakazi wa Buharamulo na hususan Nyakanazi, center kubwa inayokuwa pale?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na kipenzi cha Wanabiharamulo, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Nimhakikishie kwamba Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha Wanabiharamulo wanapata maji. Kwa hiyo, juu ya ombi lake la kuongeza mtandao, tupo tayari kutoa fedha kwa ajili ya uongezaji wa mtandao wananchi wake waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni juu ya ujenzi huu wa mradi mkubwa. Ujenzi wa mradi huu chanzo tunachukua pale eneo la Chato na ni miongoni mwa miradi ya miji 28 na mkandarasi amekwishapatikana, advance payment imekwisha tolewa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba safari moja huanzisha mwingine, uanzaji wa mradi huu ndiyo tunakwenda kukamilisha ujenzi wa mradi wa Biharamulo, ahsante sana.
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza niishukuru Serikali kupitia Mheshimiwa Waziri hapo, nimefuatilia leo na kupata uhakika kwamba mafundi sanifu wako site kwa ajili ya mradi huu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Tarafa hii ya Mzenga, na hususan Kata hii ya Mzenga, zikiwemo Kata za Vihingo, Kurui na Mafizi, zina shida kubwa ya maji, licha ya kwamba Serikali mmetoa commitment.

Je, ni namna gani Serikali inaweza kutusaidia kwa dharura ikizingatia tumeshapata lile gari la kuchimba visima? Na tunaishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali yetu ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, imefanya miradi mingi ya maji Mkoa wetu wa Pwani na Tanzania kwa ujumla.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kuweza kupunguza gharama za kuunganisha maji, hasa vijijini, ili wanawake watumie maji majumbani ili iweze kuleta tija ya miradi mikubwa iliyofanyika? Ahsante sana.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyowapigania wananchi katika Mkoa wa Pwani. Kubwa ambalo nataka nisisitize ni kwamba Mheshimiwa Rais ametupatia fedha juu ya ununuzi wa mitambo na mitambo tumekwisha inunua, niwaelekeze watu wa DDCA wafike katika haya maeneo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyaomba ili tuweze kufanya tafiti za haraka na kuhakikisha visima hivi vinachimbwa wananchi hawa waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, amezungumza juu ya gharama za maunganisho, hasa kwa wananchi kupata maji majumbani. Tumekwishatoa maelekezo katika Wizara ya Maji na watendaji wanalifanyia kazi. Tunataka tuwe na bei elekezi, hasa juu ya maunganisho ya maji majumbani. Kwa hiyo tunalifanyia kazi na tumelipokea kuhakikisha kwamba gharama zake zinakuwa reasonable na wananchi waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kata ya Mpare yenye vijiji vinne na chanzo kizuri cha maji hakuna kijiji hata kimoja chenye maji. Ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji kwenye Kata ya Mpare?

Swali la pili, mradi wa maji wa Goha, Mkumbara mkandarasi wake amekuwa akisuasua na kwa muda mrefu kazi zimesimama. Pamoja na maelekezo uliyotoa Mheshimiwa Waziri hakuna kinachoendela. Ni nini kauli Serikali juu ya mradi huu? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayofanya, lakini kubwa ambalo nataka nimhakikishie hasa katika hii Kata ya Mpare katika bajeti yetu hii ambayo tunakwenda 2023/2024 tumezingatia ombi lake katika kuhakikisha wananchi wanapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, juu ya mradi huu ambao Mkandarasi ana suasua nilishafanya ziara Korogwe, moja ya maelekezo ambayo tumeyatoa mkandarasi yule aondolewe mara moja pale site na kazi ile tutaifanya kupitia wataalam wetu na kuweza kukamilisha kazi kwa wakati. (Makofi)
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto ya upatikanaji wa maji katika Kata ya Kikolo na Kilimani pia Vijiji vya Mtama, Tukuzi, Masmeli na Mateka. Ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kujenga miradi katika maeneo hayo? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge, Jumatano kwa maana ya Tarehe 10 nawasilisha Bajeti yetu ya Wizara ya Maji kwa hiyo mambo yatakuwa ni fire, mambo ni moto. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuwa muwazi na kukiri kwamba tunayo changamoto ya maji kwenye Jimbo la Momba. Nitauliza maswali ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali inawasilisha mpango wa bajeti hapa walisema upatikanaji wa maji vijijini ni asilimia 78, na Mheshimiwa Waziri amekiri hapa kwamba tunayo adha ya maji; je, kwa kuwa anaenda kuanzisha Mradi wa Mto Momba, ipi commitment yake kwamba, mwaka wa bajeti unaokuja nasi tutafikia asilimia 78 kama wenzetu wa vijijini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Tarehe 11 Novemba, 2022 Mheshimiwa Rais wakati anazindua vifaa vipya vya kisasa vya uchimbaji, yapo maneno kadhaa ambayo alimweleza Mheshimiwa Waziri, nami sitaki kuyarejea, kwani anakumbuka, kwamba hatavumilia kuona wataalam wanaendelea kusema wamefanya utafiti na hawajaona maji. Momba hayo mambo yanaendelea, kila wakienda kufanya utafiti hawaoni maji: Ipi kauli ya Mheshimiwa Waziri kudhibitisha yale maneno ya Mheshimiwa Rais siku ya tarehe 11 Novemba, 2022?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyowapigania wananchi wake wa Momba. Maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kwamba tunakwenda kutumia rasilimali toshelevu kwa ajili ya kutatua matatizo ya maji. Vivyo hivyo sasa tunakwenda kutumia Mto Momba kwa ajili ya kutatua tatizo la maji Momba, na maji yale yatakwenda mpaka Tunduma ili wananchi wale waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni juu ya suala zima la utafiti. Nikiri miaka ya nyuma tulikuwa na changamoto juu ya vitendea kazi. Mheshimiwa Rais ametupatia fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa ambavyo vitaweza kufanya tafiti na kuhakikisha rasilimali za maji zilizokuwa chini ya ardhi zinatumika na kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya majisafi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba hata yale magari ya Mheshimiwa Rais ambayo tumeyapata katika kila mkoa, hivi ninavyozungumza lipo katika Jimbo lake la Momba katika kuhakikisha tunachimba visima na wananchi wake wanapata huduma ya majisafi na salama. (Makofi)
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafsi ya kuuliza swali la nyongeza. Lakini pia nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa utekelezaji wa hiyo miradi. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi zake nzuri. Alifika Mbinga, na wakati huo amekuja kukagua vyanzo vya maji aliona hali halisi ya mahitaji ya maji katika Mji wa Mbinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja la nyongeza. Pamoja na Serikali kusema kwamba imeanza kufanya ukarabati kilometa 21 na kununua dira za maji 2,500 kiwango hiki bado ni kidogo. Nilitaka nijue, sasa Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha ili kuhakikisha kwamba ukarabati ule unaendelea katika Mji wa Mbinga? Ahsante.
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Mbinga kwa kazi kubwa na namna ambavyo anawapigania wananchi wake. Nataka nimhakikishie na ukisoma maandiko ya dini kwa maana ya Mathayo 7:7 yanasema: “Ombeni nanyi mtapewa, bisheni hodi nanyi mtafunguliwa.”

Nataka nimhakikishie tutaiangalia Mbinga kwa namna ya pekee ili kuhakikisha wananchi wake wanapata maji. Ahsante sana.