Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Jumaa Hamidu Aweso (167 total)

MHE. MAHMOUD H. MGIMWA aliuliza:-
Mwaka 2013 Waziri Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Pinda, aliahidi kutoa shilingi 295,000,000 kwa ajili ya kusaidia ukamilishaji wa mradi wa umwagiliaji uliopo katika Kijiji cha Nundwe, Kata ya Ihalimba.
Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi hii ya Waziri Mkuu Mstaafu ili vijana walio wengi wapate ajira?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu. Lakini la pili, nimshukuru sana Rais wangu, Dkt. John Pombe Magufuli, lakini pamoja na wewe na Waheshimiwa Wabunge wote, kwa ushirikiano wote mnaonipa kipindi ambacho nipo Bungeni hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ahadi ya Waziri Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, ilianza kutekelezwa mwaka 2014 kwa Serikali kutoa kiasi cha shilingi milioni 101 ikiwa ni sehemu ya ahadi ambapo fedha fedha hizo zilitumika kujenga banio la Skimu ya Umwagiliaji ya Nundwe. Wakulima wa skimu hiyo waliweza kuchangia nguvukazi kwa kuchimba mfereji mkuu wenye urefu wa mita 1,500. Hata hivyo, usakafiaji wa mfereji mkuu kwa lengo la kudhibiti upotevu wa maji haujafanyika kwa sababu ya ufinyu wa bajeti.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa mradi huu, Wizara yangu hivi sasa inafanya mapitio ya mpango kabambe wa umwagiliaji wa mwaka 2002 ambapo miradi yote iliyoanzishwa na haijakamilika na ile inayohitaji ukarabati imepewa kipaumbele katika utekelezaji. Hivyo basi, mradi huu utaingizwa katika bajeti ya mwaka 2018/2019 kwa hatua zaidi ya utekelezaji.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza kujenga Mradi wa Maji kwa Kata ya Mtwango katika Vijiji vya Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Sawala, Mtwango, Rufana na Kibao katika Kata ya Mtwango ni miongoni mwa vijiji 12 vilivyopendekezwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi kupatiwa huduma ya maji kupitia Programu Ndogo ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini. Utelekezaji wa mradi ulipangwa kufanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Ujenzi wa mradi huo ulianza tarehe 01 Juni, 2015 na ulitakiwa kukamilika tarehe 01 Juni, 2016 kwa gharama ya shilingi bilioni 2.36. Awamu ya kwanza ilikuwa ni ujenzi wa miundombinu ya maji katika Kijii cha Sawala pekee ambapo hadi sasa ujenzi umefikia asilimia 50.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwezi Novemba 2016 mkandarasi alikuwa hajakamilisha kazi na hivyo Halmashauri kuamua kuvunja mkataba. Halmashauri ilitangaza upya zabuni kwa ajili ya ukamilishaji wa kazi zilizobaki. Mkandarasi mwingine amepatikana na utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kuanza mwezi Desemba, 2017 kwa muda wa miezi 12 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.81. Serikali katika mwaka wa 2017/2018 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.56 kwa ajili ya Halmashauri ya Mufindi ili kukamilisha mradi huo katika Vijiji vyote vya Sawala, Mtwango, Rufuna na Kibao na kuendelea na utekelezaji wa miradi mingine ya vijijini.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-
Serikali kupitia Mradi wa Vijijini kumi unaofadhiliwa na Benki ya Dunia iliahidi kupeleka maji Maretadu, Labay, Gidmadoy, Qamtananat, Garbabi, Magana Juu na Qatabela:-
Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya utekelezaji wa ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji katika Halmashauri zote nchini. Utekelezaji wa programu hii unafanyika kwa awamu. Katika awamu ya kwanza ya utekelezaji kwa Halmashauri ya Mbulu Vijiji vya Singu, Masieda, Arri-Harsha, Dongobesh, Mongahay, Tumati, Haydom na Moringa vilihusika. Hadi sasa miradi ya maji katika Vijiji vya Singu na Masieda imekamilika na ujenzi unaendelea katika vijiji vilivyobaki. Serikali katika kuhakikisha inakamilisha miradi ya maji na kuanzisha mingine mipya kiasi cha shilingi bilioni 2.09 zimetengwa kwa Wilaya hiyo katika mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu ya pili ya utekelezaji wa WSDP iliyoanza Julai, 2016, Halmashauri zote nchini ikiwemo ya Mbulu zimewasilisha mipango ya utekelezaji wa miradi kwa kipindi cha miaka mitano (5) kwa maana 2016/2017 - 2020/2021 ambapo miradi mingi ya maji itatekelezwa kulingana na mpango huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu vilivyopo katika mpango huo ni Maretadi, Labay, Didmadoy, Quantananat, Garbabi, Magana Juu na Qutabela. Kwa kuanzia Vijiji vya Meretadu, Labay na Garbabi vimepewa kipaumbele katika mwaka wa fedha 2017/2018 ikiwa ni pamoja na Vijiji vya Genda, Ng’orat na Endahagichan. Vijiji vingine katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu vitaendelea kutekelezwa kutegemeana na upatikanaji wa fedha.
MHE. KIZA H. MAYEYE aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma umebarikiwa kuwa na Ziwa Tanganyika, Mto Malagarasi na vyanzo vingine vya maji lakini Mkoa huu unakabiliwa na changamoto kubwa ya maji.
Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Kigoma hususan katika Jimbo la Kigoma Kaskazini katika kuhakikisha wanapata maji ya kudumu ya kwenye mabomba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiza Hussein Mayeye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji inaendelea kutekeleza miradi wa maji vijijini katika Halmashauri ya Wilaya Kigoma iliyopo Kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma. Hadi kufikia mwezi Septemba, 2017 jumla ya miradi mitatu ya maji ya Nyarubanda, Kagongo na Nkungwe imekamilika na wananchi wanapata huduma ya maji. Mradi mmoja wa Kalinzi upo katika hatua za mwisho na utekelezaji wake umefika asilimia 90. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri hiyo imetengewa shilingi milioni 649.8 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi ya maji vijijini.
Vilevile Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Ubeligiji imeanza utekelezaji wa miradi ya maji katika vijiji vya Halmashauri za Mkoa wa Kigoma utakaogharimu shilingi bilioni 20.6 na itatekelezwa katika kipindi cha miaka minne kuanzia mwaka 2017 hadi 2021. Mradi huo utanufaisha wakazi 207,785 katika vijiji 26 vya kipaumbele katika Halmashauri za Mkoa huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa mijini, Serikali inatekeleza mradi wa maji Mjini Kigoma kwa gharama ya Euro milioni 16.32. Mradi huo unahusisha ujenzi wa chanzo cha maji ukingoni mwa Ziwa Tanganyika eneo la Amani Beach chenye uwezo wa kuzalisha maji lita milioni 42 kwa siku, ikilinganishwa na lita milioni 12 zinazozalishwa sasa. Kazi nyingine zitakazofanyika ni pamoja na ujenzi wa matanki matano yenye ujazo wa lita milioni mbili kila moja na tanki moja lenye ujazo wa lita 500,000; ulazaji wa bomba kuu lenye urefu wa kilometa 22 na mabomba ya kusambaza maji urefu wa kilometa 132, ujenzi wa vioski 70 vya kuchotea maji katika maeneo mbalimbali.
Aidha, katika kuboresha huduma ya usafi wa mazingira, mabwawa ya kutibu majitaka yenye uwezo wa kutibu mita za ujazo 150 kwa siku yatajengwa pamoja na ununuzi wa gari la kunyonya na kusafirisha majitaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia mwezi Oktoba 2017, kwa ujumla utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia
76 na unatarajiwa kukamilika mwezi Disemba 2017. Kukamilika kwa mradi huo kutaongeza upatikanaji wa majisafi na salama kutoka asilimia 69 za sasa hadi kufikia asilimia 100.
MHE. SEIF K. GULAMALI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaamua kubadili mita zote za maji ili wananchi wanunue maji kwa mfumo wa unit wao wenyewe kama ilivyo kwenye umeme?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali, Mbunge wa Manonga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo sugu la baadhi ya wateja wa Mamlaka za Maji kutolipa ankara za maji na kulimbikiza madeni, Wizara yangu inafanya majaribio ya kutumia mfumo wa malipo kabla ya huduma yaani prepaid system. Kupitia mfumo huo, mteja hufungiwa kifaa maalum kinachomwezesha kulipia kwanza kiasi cha maji anachohitaji kabla ya kutumia. Hata hivyo, mfumo huo una gharama kubwa kiuwekezaji na kimatunzo ikilinganishwa na mfumo unaotumika sasa. Kwa sababu hiyo ya gharama Wizara imeagiza baadhi ya Mamlaka kuzifunga mita hizo kwa wateja wake wenye tabia ya kulimbikiza madeni ya ankara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwezi Oktoba, 2017 jumla ya Mamlaka za maji saba zimeanza kutumia mfumo huo kwa baadhi ya wateja wao. Mamlaka hizo ni za Miji ya Makao Makuu ya Mikoa ya Iringa, Arusha, Dodoma, Mbeya, Songea, Tanga na DAWASCO ya Jiji la Dar es Salaam. Mpaka sasa mfumo umeonesha mafanikio makubwa. Hata hivyo, kutokana na ukubwa wa gharama za mfumo huo, Wizara imeziagiza Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira za Daraja ‘A’ zinategemea kwa gharama zote za uendeshaji kuhakikisha kuwa zinatenga fedha katika bajeti zao ili kuwezesha kuendelea na ufungaji wa mfumo huo kwa kadri hali ya kifedha itakavyoruhusu.
MHE. MUSA R. NTIMIZI aliuliza:-
Serikali imeanza mchakato wa kutoa maji ya Ziwa Victoria kupeleka katika Mkoa wa Tabora:-
• Je, mradi huo utapita katika Wilaya ya Uyui?
• Je, ni vijiji gani katika Jimbo la Igalula vitanufaika na mradi huo hasa ukizingatiwa shida kubwa ya maji waliyonayo wananchi hao?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Jimbo la Igalula lenye vipengele (a) na kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali tayari imeanza kutekeleza mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika Miji ya Tabora, Igunga, Nzega na Uyui pamoja na Vijiji 89 vilivyopo umbali wa kilomita 12 kila upande kutoka bomba kuu. Katika mradi huo bomba la kupeleka maji katika Manispaa ya Tabora kutoka Mjini Nzega linapita katika Wilaya ya Uyui, ambapo jumla ya Vijiji 15 vitanufaika na mradi huo. Vijiji hivyo ni Upuge, Mhongwe, Lunguya, Kasenga, Magiri, Imalampaka, Kalemela, Ilalwasimba, Isikizya, Igoko, Ibushi, Ibelemailudi, Mtakuja, Itobela na Isenegeja.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Jimbo la Igalula, Vijiji vyake vipo umbali unaozidi kilomita 12 kutoka bomba kuu. Vijiji hivyo vitaingizwa katika utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji Awamu ya Pili iliyoanza kutekelezwa mwezi Julai, 2016.
MHE. GIBSON B. MEISEYEKI aliuliza:-
Uhaba wa maji ni moja kati ya matatizo sugu katika Jimbo la Arumeru Magharibi ingawa maji yote yanayotumika katika Jiji la Arusha yanatokea kwenye Jimbo la Arumeru Magharibi:-
Je, ni nini mkakati wa haraka wa Serikali wa kutatua tatizo hilo la maji katika kata takribani 20 kati ya kata 27 za jimbo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gibson Blasius Meiseyeki, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli zaidi ya asilimia 65 ya maji yanayotumika Jiji la Arusha yanatoka katika vyanzo vilivyopo katika Halmshauri ya Arusha lilipo Jimbo la Arumeru Magharibi. Mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP) ni kuboresha huduma ya maji vijijini na mijini kwa kujenga miradi mipya, kupanua na kukarabati miundombinu ya maji.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa Serikali imekamilisha miradi mitatu katika Vijiji vya Ilkirevi, Oleigeruno na Nduruma na miradi mingine sita katika Vijiji vya Bwawani, Likamba, Ngaramtoni, Oloitushula, Nengun’gu na Loovilukuny ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Miradi yote hiyo ipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Kata za Moivo, Sokon II, Kiranyi, Bangata na Kiutu ambazo zipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha vinanufaika na huduma ya maji safi na salama yanayotumika katika Jiji la Arusha. Aidha, Kata tatu za Olturumet, Olmotony na Kimnyak ambazo pia zipo katika Halmashauri hiyo zitanufaika na mradi mkubwa wa maji unaotekelezwa hivi sasa katika Jiji la Arusha.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2017/ 2018, Serikali imetenga shilingi bilioni tatu kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Arusha za kukamilisha miradi inayoendelea. Aidha, hivi sasa Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Uingereza kupitia Shirika la Kimataifa la Maendeleo (DFID) imetoa shilingi bilioni 3.5 kwa ajili ya usanifu wa mradi wa kuboresha huduma ya maji utakaohudumia Vijiji vya Lengijave, Olkokola, Ekenywa, Ngaramtoni na Seuri ambavyo pia vipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha. Usanifu wa mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018.
MHE. ZAINAB M. AMIR aliuliza:-
Mboga za majani ni lishe bora kwa afya ya binadamu na wakulima wengi wa mbogamboga katika Jiji la Dar es Salaam wanatumia maji yasiyo salama kwa ajili ya kumwagilia na huenda maji hayo yana kemikali zinazoweza kusababisha mbogamboga hizo kudhuru afya za wananchi badala ya kuziimarisha:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia maji safi na salama wakulima hao wa mbogamboga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amir, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kuzingatia umuhimu wa afya za wananchi inaendelea kutoa miongozo na ushauri kuhusu maji yanayofaa kwa matumizi ya binadamu na kwa shughuli za uchumi. Katika kuhakikisha wananchi wanalima mbogamboga katika maeneo sahihi, Serikali iliunda Kikosikazi kwa kushirikisha Maafisa wa Baraza la Mazingira la Taifa (NEMC).
Mheshimiwa Spika, kikosi hicho kilitembelea baadhi ya mito iliyopo Dar es Salaam na kugunda uchafuzi mkubwa wa mazingira unaosababishwa na utiririshaji wa maji taka kutoka majumbani na kwenye viwanda na hivyo maji hayo kuwa na kemikali zisizofaa kwa matumizi ya kilimo cha mbogamboga, kwa mfano maji ya Mto Msimbazi.
Mheshimiwa Spika, Serikali inawakataza wananchi kulima mbogamboga katika maeneo hayo yenye uchafuzi kwa kuwa maji hayo yana athari kwenye afya. Aidha, kwa kuwa suala hili ni mtambuka na linahusu uchafuzi wa mazingira, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, inaendelea kupima maji ya mito hiyo na kutoa taarifa za hali ya maji. Pia halmashauri za manispaa katika Jiji la Dar es Salaam zinashauriwa kutunga na kusimamia sheria ndogo kwa ajii ya kudhibiti uchafuzi wa maji ya mito hiyo.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kufanya shughuli zao za kilimo cha umwagiliaji, ikiwemo umwagiliaji wa mbogamboga katika maeneo sahihi.
MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza:-
Kwa muda mrefu chanzo cha maji cha Ruvu Chini na Ruvu Juu kimekuwa chanzo pekee cha maji katika Mkoa wa Pwani. Lakini kimsingi chanzo hicho hakitoshelezi mahitaji na hivyo kushindwa kumaliza tatizo la maji.
Je, ni lini Serikali itatumia chanzo cha maji cha Mto Rufiji kuwapatia maji safi na salama wananchi hususan wa Wilaya ya Rufiji, Kibiti, Mkuranga na Kisarawe?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika,kwa Niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Kuanzia mwaka 2005 hadi 2007 Serikali ilifanya uchunguzi wa vyanzo 26 vya maji kwa ajili ya matumizi ya Jiji la Dar es Salaam na Miji ya Kibaha na Bagamoyo kwa miaka 2025 hadi 2032. Uchunguzi huo ulibaini kuwa wakati ule vyanzo vya maji vya mto Ruvu na visima vya Kimbiji na Mpera vilikuwa vinatosha kwa matumizi ya Jiji la Dar es Salaam na maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Pwani hadi mwaka 2032. Chanzo cha maji cha Mto Rufiji hakikuchaguliwa wakati huo kwa sababu ilionekana gharama za kusafisha na kusafirisha maji kutoka Mto Rufiji hadi Dar es Salaam zilikuwa kubwa ukilinganisha na vyanzo vingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati uchunguzi huo unafanyika, Serikali ilifanya uchunguzi wa vyanzo mbadala kwa ajili ya miji ya Utete, Ikwiriri, Mkuranga na Kisarawe. Uchunguzi ulibaini kuwa miji hiyo inaweza kupata maji ya visima. Miradi mikubwa ya visima ilitekelezwa katika miji hiyo na kunufaisha wakazi wa maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kukidhi mahitaji ya maji kwa Jiji la Dar es Salaam pamoja na maeneo ya Mkoa wa Pwani hususan Wilaya za Rufiji, Kibiti, Mkuranga na Kisarawe, Serikali imeanza taratibu za kumwajiri mtaalam mshauri kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na utayarishaji wa vitabu kwa kutumia chanzo cha Mto Rufiji. Kazi hiyo inatarajiwa kuanza mwaka wa fedha 2018/2019. Ahsante.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:-
(a) Je, lini mradi wa maji ya kutoka Mto Kagera utaanza kuhudumia wananchi wa Kyaka na Bunazi?
(b) Je, mradi huo utagharimu kiasi gani cha fedha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Dkt. Diodorus Buberwa Kamala, Mbunge wa Nkenge, kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Bukoba (BUWASA) imeanza utekelezaji wa mradi wa kutoa maji Mto Kagera kwenda kwenye Miji ya Kyaka na Bunazi. Kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa makabrasha ya zabuni za ujenzi inaendelea na inatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, 2018. Ujenzi wa mradi huo unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama halisi za utekelezaji wa mradi huo zitajulikana ifikapo mwezi Septemba, 2018 baada ya kukamilika kwa usanifu unaoendelea.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Jimbo la Mlimba lina mito mikubwa inayotiririka mwaka mzima kwa miaka mingi, lakini Jimbo limekuwa na tatizo kubwa la kupata maji safi na salama.
(a) Je, ni lini Serikali itatumia uwepo wa mito hiyo kama fursa ya kuwapatia maji safi na salama wananchi wa Mlimba hasa Mji Mdogo wa Mlimba?
(b) Je, ni lini Serikali itatumia uwepo wa mito hiyo kujenga mabwawa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwajiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Jimbo la Mlimba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tayari imeanza kutumia fursa ya mito iliyopo katika Jimbo la Mlimba kuwapatia maji safi na salama wananchi wa Jimbo hilo. Mpaka sasa kuna miradi minne ya Tanganyika Masagati, Chita/Ching’anda, Mngeta/Mchombe na Mkangawalo/ Kidete/Itongowa. Vyanzo vyake ni mito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika bajeti ya mwaka 2017/2018 Serikali imepanga kujenga mradi wa maji Mbingu/Vigaeni ambao chanzo chake ni Mto Ifumbo. Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero imepanga kufanya usanifu wa kupeleka maji katika Kata ya Mlimba kwa kutumia Mito ya Mgugwe na Mpanga, kwa sasa mji mdogo wa Mlimba unapata huduma ya maji kupitia visima virefu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa ujenzi wa mabwawa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Kuanzia mwaka 2013/2014 hadi 2015/2016, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Marekani kupitia Shirika lake la Maendeleo (USAID) ilifanya upembuzi yakinifu katika Bonde la Mto Kilombero ikiwemo maeneo ya Jimbo la Mlimba kwa ajili ya kubainisha maeneo ya kujenga skimu za umwailiaji na mabwawa ambapo takribani hekta 43,000 zilibainishwa. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya uendelezaji maeneo hayo.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-
Jimbo la Lushoto linakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji hususan katika maeneo ya Ubiri, Makanya, Kwemashai, Gare, Mlola, Mbwei, Malibwi na Kilole:-
Je, ni lini Serikali itawapatia wananchi hao majisafi na salama ili waondokane na adha hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omar Shekilindi, maarufu kama Bosnia, Mbunge wa Jimbo la Lushoto, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Vijij vya Ubiri, Makanya, Kwemashai, Gare, Mlola, Mbwei, Malibwi na Kilole. Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi katika vijiji hivyo ambapo kwa mradi wa Mlola ujenzi wake umefika 85%; miradi ya maji katika maeneo ya Kwemashai na Ngulu imefikia 75%; wakati mradi wa maji Malibwi umekamilika na wananchi wanapata huduma ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji wa Ubiri ulijengwa Mwaka 1972 ili kuwahudumia wakazi 2,013. Hata hivyo kutokana na ongezeko la wakazi huduma ya maji inayotolewa kwa sasa haitoshelezi mahitaji. Hivyo Halmashauri ina mpango wa kutoa maji kutoka Kijiji cha Ngulu pindi mradi wa kijiji hicho utakapokuwa umekamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Gare ambao ulijengwa na Wamisionari Mwaka 1978 haukidhi mahitaji ya sasa, hivyo Halmashauri imeuweka kwenye mpango wa kuufanyia upanuzi na usanifu wa kina ili kuuongezea uwezo na idadi ya vituo vya kuchotea maji. Aidha, miradi katika Vijiji vya Makanya, Kilole na Mbwei imewekwa katika mpango wa utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji awamu ya pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa lengo la kuwaondolea adha ya upatikanaji wa maji wananchi wa Halmashauri ya Lushoto, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.66 kwa ajili ya Halmashauri hiyo kukamilisha miradi inayoendelea kutekelezwa pamoja na kuanzisha miradi mipya.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-
Wilaya ya Liwale ina miradi mikubwa miwili ya umwagiliaji, Mradi wa Ngongowele na Mtawango lakini Mradi wa Ngongowele umesimama kwa muda mrefu sasa.
(a) Je, ni nini hatma ya mradi huu wa Ngongowele kwa sasa?
(b) Je, Serikali iko tayari kumpeleka Mkaguzi wa Hesabu za Serikali ili kukagua mradi huu ambao unaonekana kuhujumiwa kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka, Mbunge wa Jimbo la Liwale, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya kwanza wa Mradi wa Ngongowele ilianza kutekelezwa mwaka 2009 kwa kujenga banio na miundombinu yake kwa gharama ya shilingi milioni 346.1 kupitia Mfuko wa Kuendeleza Umwagiliaji ngazi ya Taifa. Awamu ya pili wa mradi ilitekelezwa mwaka 2010 kwa gharama ya shilingi milioni 400. Kazi zilizofanyika ni kuchimba na kusakafia mfereji mkuu mita 2,500; kujenga vigawa maji sita; kujenga makalvati matano; kujenga kujenga kivusha maji chenye urefu wa mita 80 na kuchimba mfereji wa kutoa maji mita 200. Awamu hii ya utekelezaji ilikumbwa na changamoto ya mafuriko makubwa yaliyotokea katika maeneo hayo na kuharibu miundombinu. Hali hiyo ilipelekea mkandarasi kuongezewa muda wa kukabidhi kazi kutoka tarehe 01.10.2011 hadi tarehe 30.10.2011. Baada ya kushindwa kukabidhi kazi kwa tarehe hiyo, Halmashauri ilianza kumkata liquidated damage ya asilimia
0.15 ya thamani ya mkataba wa siku kwa muda wa siku 100 hadi tarehe 15.02.2012 na baadaye ilivunja mkataba kutokana na mkandarasi huyo kushindwa kukabidhi kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa mradi huo kwa wananchi wa Ngongowele na Taifa kwa ujumla, Serikali kupitia mradi wa kuendeleza skimu ndogo za wakulima itatenga fedha katika mwaka wa fedha 2018/ 2019 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa mradi huu ili ufanye kazi. Aidha, Serikali itafuatilia utekelezaji wa Mradi wa Ngongowele na endapo itabainika kuna hujuma katika utekelezaji wa mradi huo hatua stahiki zitachukuliwa.
MHE. DANIEL E. MTUKA aliuliza:-
Bwawa linalotarajiwa kuchimbwa katika Kijiji cha Mbwasa, Tarafa ya Kitinku ni la kimkakati kwa wakazi wa Tarafa nzima ya Kintinku.
Je, ni lini Serikali itaanza rasmi ujenzi wa bwawa hilo baada ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Edward Mtuka, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2012/2013 Halmashauri ya Manyoni ilipanga kujenga Bwawa la Mbwasa kwa kupitia Mto wa Msimu wa Liula ikiwa ni hitaji la wananchi wa Kijiji cha Mbwasa kwa ajili ya shughuli za kilimo, mifugo na matumizi ya nyumbani. Ujenzi wa Bwawa la Mbwasa ulikusudiwa kunufaisha pia wananchi wa vijiji jirani vya Mwiboo, Mtuwe na Chikuyu, lengo kuu likiwa na kuimarisha kilimo cha umwagiliaji wa zao la mpunga. Hali hii inatokana na maeneo hayo kutokuwa na uhakika wa mvua za kutosha kwa ajili ya uzalishaji wa mazao ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2012/2013 upembuzi yakinifu na usanifu wa Bwawa la Mbwasa ulifanyika kupitia Ofisi ya Umwagiliaji wa Kanda ya Dodoma. Aidha, matokeo ya upembuzi huo yalibaini kuwa jumla ya shilingi bilioni 2.5 zingehitajika kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hilo.
Mheshimiwa Mwenyiti, katika mwaka wa fedha 2016/ 2017 Wizara yangu kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ilianza kufanya mapitio ya Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa mwaka 2002 kwa kutambua umuhimu wa ujenzi wa mabwawa kama hatua ya kimkakati ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Katika kuwezesha kilimo cha uhakika katika maeneo kame, Bwawa la Mbwasa litapewa kipaumbele katika bajeti ijayo ya mwaka wa fedha 2018/2019 kwa ajili ya kuanza utekelezaji.
MHE. LATHIFAH H. CHANDE aliuliza:-
Halmashauri ya Mji wa Liwale imetumia takribani shilingi milioni 540 katika ujenzi wa mradi wa umwagiliaji katika Kata ya Mtawango, lakini mradi huo umejengwa chini ya kiwango na hakuna thamani ya matumizi ya fedha (value for money).
Je, Serikali ipo tayari kwenda kukagua mradi huo na kufanya uchunguzi ili kubaini kasoro za mradi huo na kuwawajibisha wote watakaobainika kuuhujumu mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:- Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lathifah Chande, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa umwagiliaji wa Mtwango upo katika kijiji cha Mtawango, Kata ya Mbaya, Tarafa ya Liwale, Halmashauri ya Wilaya ya Liwale. Mradi huu uliibuliwa nawananchi mwaka 2008 na una jumla ya eneo la hekta 230.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua za uboreshaji zilianza mwaka 2009 kwa kufanya upimaji na usanifu wa awali. Katika mwaka 2011/2012 mradi huo ulitengewa fedha kiasi cha shilingi milioni 220 kupitia Mfuko wa Wilaya wa Kuendeleza Kilimo cha Umwagiliaji kwa ajili ya ujenzi wa banio, uchimbaji wa mfereji mkuu mita 1,000, ujenzi wa vigawa maji vinne. Kazi hizo zilifanyika na kukamilika kulingana na matakwa ya mkataba.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014 mradi ulitengewa fedha kiasi cha shilingi milioni 184 kwa ajili ya kusakafia mfereji uliochimbwa na mita 1,000 kujenga vigawa maji nane, kujenga ukuta wenye urefu wa mita 250 kwa ajili ya kukinga mafuriko, kujenga kivusha maji na kivuko kwa ajili ya watembea kwa miguu na mitambo. Kazi hizo zilifanyika na kukamilika kulingana na matakwa ya mkataba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kasoro alizobainisha Mheshimiwa Mbunge, Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, itaunda timu ya wataalam kwa ajili ya uchunguzi na endapo itabainika kweli kuna hujuma katika mradi huo, hatua stahiki zitachukuliwa kwa wahusika.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Mwaka 2014/2015 Serikali iliahidi kuongeza usambazaji maji katika vijiji 100 vilivyoko umbali wa kilometa 12 kutoka bomba kuu la Ziwa Victoria hadi Kahama na Shinyanga na Serikali ilishatenga shilingi bilioni nne ili kutekeleza mradi huo.
(a) Je, vijiji vingapi vimeshapatiwa maji kati ya hivyo 100 hadi sasa?
(b) Je, Serikali itafikisha lini maji ya Ziwa Victoria katika Vijiji vya Mwakazuka, Mwaningi, Kabondo, Ntundu, Busangi, Buchambaga, Nyamigege, Gula, Izuga, Buluma, Matinje na Bubungu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Maige, Mbunge wa Msalala lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inatekeleza mradi wa maji wa vijiji 100 vilivyopo kandokando ya bomba kuu kutoka Ziwa Victoria hadi Kahama, Shinyanga. Utekelezaji wa mradi huo unafanywa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Katika awamu ya kwanza jumla ya vijiji 40 vilivyopo katika Halmshauri za Msalala, Misungwi, Kwimba na Shinyanga vimetambuliwa na ujenzi wa miradi ya maji ambapo katika vijiji 33 umekamilika na baadhi ya vijiji vingine vinaendelea na ujenzi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyotajwa juu ni miongoni mwa vijiji 100 vilivyotambuliwa. Tayari halmashauri ya Msalala imekamilisha usanifu wa kina kwenye vijiji vya Ntundu, Busangi, Nyamigege, Gula, Ntobo, Masabi na Chela. Aidha, vijiji vya Mwakazuka, Kabondo na Izuga zabuni zake zimeshatangazwa na KASHWASA na tayari mkandarasi amepatikana. Vijiji vya Mwaningi, Buchambaga, Buluma, Matinje na Bubungu vipo katika hatua za awali za utekelezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga na kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji katika vijiji vinavyoendelea na vilivyobaki kulingana na bajeti ilivyotengwa.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-
Upungufu wa maji safi na salama kwa matumizi ya binadamu na mifugo ni moja ya kero kubwa kwa wananchi wa Wilaya ya Longido. Vyanzo vya maji vilivyoko ni vichache na ni vya muda (seasonal) na mahali pengine hakuna kabisa:-
(a) Je, utekelezaji wa mradi mkubwa wa kuleta maji ya bomba kutoka Mto Simba ulioko Siha, Mkoani Kilimanjaro hadi Mji wa Longido kilometa 64 unaogharimu shilingi bilioni 16 umefikia hatua gani?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuendeleza usambazaji wa maji hayo ili yawafikie wananchi wapatao 23,000 waishio katika Kata Kimokouwa na Namanga pia Kiserain ambazo zipo umbali wa kuanzia kilometa 15 - 25 tu toka Longido Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Mbunge wa Longido, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza mradi wa uboreshaji wa huduma ya upatikanaji wa maji katika Mji wa Longido. Mradi huo umegawanyika katika vipande vinne. Utekelezaji wa kipande cha kwanza unagharimu shilingi bilioni
• Hadi mwezi Machi 2018, utekelezaji wa kipande hicho umefikia asilimia 15. Utekelezaji wa kipande cha pili unagharimu shilingi bilioni 2.54.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi mwezi Machi 2018 utekelezaji wa kipande hicho umefikia asilimia 40. Kipande cha tatu kinagharimu shilingi milioni 276.36. Hadi mwezi Machi 2018 utekelezaji wa kipande hicho umefikia asilimia 90. Kipande cha nne kinahusu ulazaji wa mabomba ya usambazaji maji katika Mji wa Longido kwa gharama ya shilingi bilioni 2.09 ambapo utekelezaji wa kipande hicho umefikia asilimia 85.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu umesanifiwa kutoa huduma kwa Kata za Longido, Engikaret na Orbomba zenye jumla ya wakazi 16,712 kwa takwimu ya sensa ya watu wa makazi ya mwaka 2012, ambapo Kata ya Longido ina wakazi 2,285; Kata ya Orbomba 7,900; na Engikaret ya wakazi 6,527; na inatazamiwa idadi ya watu ikafika 26,145 kwa Kata zote tatu ifikapo mwaka 2024 kwa ongezeko la asilimia 3.8 kwa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Kata za Kimokouwa, Namanga na Kiserian zitaingizwa katika mpango wa awamu ya pili ya uzambazaji maji baada ya mradi huu kukamilika.
MHE. MARWA R. CHACHA (K.n.y. MHE. LUCY F. OWENYA) aliuliza:-
Mradi wa Maji Vijijini katika Kata ya Old Moshi Magharibi katika Kijiji cha Mande haujatekelezwa kuanzia mwaka 2008; Je, ni sababu zipi zilizosababisha mradi huo kutokamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Fidelis Owenya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP I) Halmashauri ya Wilaya ya Moshi ilipanga kutekeleza miradi ya maji katika vijiji 12. Kati ya vijiji hivyo ujenzi wa miradi umekamilika katika vijiji sita vya Korini Juu, Korini Kati, Korini Kusini, Kilima Juu, Kilima Kati na Golo na utekelezaji wa miradi iliyobaki unaendelea kufanyika katika awamu ya pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP II).
Mheshimiwa Naibu Spika, usanifu wa mradi wa maji wa Tela Mande ulikamilika mwaka 2013. Mkandarasi aliyeteuliwa hakuweza kuanza kazi na ulichelewa kutekelezwa kutokana na ufinyu wa bajeti. Halmashauri ya Wilaya ya Moshi iliutangaza mradi huu katika mwaka wa fedha 2017/2018 na kwa sasa mradi huo upo kwenye hatua ya tathmini (evaluation) ili kumpata mkandarasi wa ujenzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, uUtekelezaji wa mradi huu unategemea kuanza mwezi Mei, 2018. Mradi huu utakapokamilika utahudumia wakazi 5,141 kulingana na sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 kwa Vijiji vya Tela na Mande.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza:-
Je, Serikali ipo tayari kutuma timu ya tathmini ya kukagua Miradi ya Maji ya Kwediboma, Kwekivu, Sange, Chamtui na Mafuleta ili kuona kama vigezo na viwango vya ujenzi wa miradi hii mikubwa vimezingatia thamani ya fedha (value for money audit)?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Jimbo la Kilindi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ya maji nchini ikiwemo maeneo ya vijijini ili kuweza kuwapatia wananchi huduma ya maji safi, salama kwa asilimia 85 ifikapo mwaka 2020. Ili miradi ya maji iweze kutekelezwa kwa ufanisi, Serikali hufanya ufuatiliaji na tathmini ili kupima matokeo ya mradi uliokamilika na unaoendelea kulingana na vigezo vitano (kufaa, kutekelezeka, ufanisi, athari na uendelevu) katika mpangilio unaoeleweka ili kusaidia kuboresha miradi mingine inayoendelea.
Mheshimiwa Spika, kufuatia ombi la Mheshimiwa Mbunge, naomba nimshukuru kwanza kwa kuona umuhimu wa kufuatilia miradi ya maji iliyoko jimboni kwake. Hivyo namhakikishia kuwa nitatuma timu ya wataalam kwa ajili ya kwenda kufanya ukaguzi wa ujenzi wa miradi hiyo ili kuona kama vigezo na viwango vya ujenzi wa miradi hiyo mikubwa vimezingatiwa.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA (K.n.y. MHE. AJALI R. AKBAR) aliuliza:-
Je, nini hatma ya Mradi wa Maji wa Makondeko?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ajali Rashid Akbar, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji imeandaa mpango madhubuti katika kuhakikisha inaboresha huduma ya maji kwa wananchi wanaohudumiwa na Mradi wa Maji wa Kitaifa wa Makonde. Katika kufikia lengo hilo, Wizara inatekeleza mipango ya muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kazi za muda mfupi, Wizara imefanya ununuzi wa mabomba ya urefu wa kilometa 24 kwa ajili ya kukarabati baadhi ya maeneo yaliyochakaa sana yenye kipenyo cha inchi mbili hadi sita, kwa maeneo ya Makote hadi Nanguruwe, Nanda hadi Kitangali, Chihangu hadi Mnyambe, Ghana Juu hadi Lukokoda na Mahuta hadi Nanywila. Aidha, ununuzi wa pampu kumi umefanyika ambazo zitafungwa katika vyanzo vitano vya kuzalisha na kusambaza maji. Matayarisho ya ulazaji wa mabomba na ufungaji wa pampu yanaendelea.
Mheshimiwa Spika, katika mpango wa muda wa kati Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo (CRIDIF) kutoka Afrika ya Kusini wametekeleza ukarabati wa visima sita ambavyo vimeongeza uzalishaji wa maji kutoka lita miloni 6.72 hadi lita milioni 11.88 kwa siku katika chanzo cha Mitema.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa CRIDIF wanaendelea na upembuzi yakinifu kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya pili ambayo itahusu ununuzi na ujenzi wa bomba kuu kutoka chanzo cha Mitema kwenda Nanda la urefu wa kilometa
8.56 lenye kipenyo cha inchi 12; ujenzi wa mtandao wa usambazaji kutoka Nanda kwenda Kijiji cha Mtopwa na ukarabati na ujenzi wa matanki ya maji katika Vijiji vya Mtopwa, Nanywila na Mtavala.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza mpango wa muda mrefu, Serikali imepanga kutumia kiasi cha dola za Kimarekani milioni 84 kutoka mkopo wa masharti nafuu wa Serikali ya India ambazo zitatumika kufanya ukarabati wa mradi mzima. Kwa sasa majadiliano kwa ajili ya kusaini mkataba wa kifedha yanaendeea kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya India.
MHE. SALUM MWINYI REHANI aliuliza:-
Serikali inatekeleza mradi mkubwa wa umeme wa Bwawa la Kidunda ambapo pia kutakuwa na miradi ya kilimo na ufugaji samaki.
• Je, kuna tathmini ya kitaalamu iliyofanyika ya kudhtibiti kemikali zinazotokana na utumiaji mkubwa wa dawa za kudhibiti magugu kwenye mashamba ya miwa na mpunga na utumiaji wa mbolea za SA ambazo husababisha uharibifu wa ardhi?
• Je, Serikali inaweza kuleta Bungeni ripoti ya tathmini pamoja na Environmental Impact Assessment juu ya mradi huo?
• Je, mradi wa umwagiliaji utachukua ekari ngapi na imepanga kulima nini katika mashamba hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salum Mwinyi Rehani, Mbunge wa Jimbo Uzini, lenye sehemu (a), (b), (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kulinga na tathmini ya athari za mazingira iliyofanyika Bwawa la Kidunda halitakuwa na athari za kikemikali za kudhibiti magugu kwenye mashamba ya miwa na mpunga kwani mashamba hayo yatakuwa upande wa chini wa bwawa yaani downstream ambapo kemikali haziwezi kurudi nyuma kuingia kwenye bwawa. Ripoti ya mazingira imeainisha athari zote zinazotarajiwa na namna ya kukabiliana nazo.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaweza kuleta Bungeni cheti cha mazingira kilichotolewa na Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuhusu mradi wa Kidunda.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Bwawa la Kidunda ni mahsusi kwa ajili kuhifadhi maji kwa matumizi ya majumbani na viwandani. Hata hivyo, kiasi cha maji lita milioni 432 kwa siku sawa na mita tano za ujazo kwa sekunde, yatatumika kwa ajili ya umwagiliaji na shamba namba 217 la Mkulazi lenye hekta 28,000 zinazofaa kwa kilimo cha miwa na mpunga.
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:-
Serikali imeahidi mradi wa maji ambao utamaliza kero ya maji katika Jimbo la Morogoro Mjini hasa maeneo ya Kihonda, Tungi, Lukobe, Mkundi katika Kata ya Mindu.
(a) Je, ni lini mradi huo wa maji utaanza ili kuondoa kero za maji katika Jimbo la Morogoro Mjini?
(b) Je, mradi huo utagharimu fedha kiasi gani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdul- Aziz Mohamed Abood, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji imeandaa mipango madhubuti katika kuhakikisha inaboresha huduma ya maji kwa wakazi wanaoishi katika Manispaa ya Morogoro. Katika kufikia lengo hilo, Wizara inatekeleza mipango ya muda mfupi na muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mpango wa muda mfupi, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitenga jumla ya shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya mradi wa kuboresha huduma ya maji kwa maeneo mbalimbali ya Manispaa ya Morogoro. Kazi zinazotekelezwa katika mradi huo ni pamoja na ujenzi wa mtandao wa usambazaji maji wenye urefu wa kilometa 41.9 na kituo cha kusukuma maji eneo la Mizani. Kukamilika kwa mradi huo kutawanufaisha wakazi wapatao 17,000 wanaoishi maeneo ya Kihonda, Kilimanjaro, Mkundi, Yespa, Kiyegea na Kihonda Kaskazini. Mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika lake la Maendeleo la AFD itatekeleza mradi wa kuboresha huduma ya majisafi katika Manispaa ya Morogoro. Kazi zinazotekelezwa katika mradi huo ni pamoja na kuongeza kina cha bwawa la Mindu, ujenzi wa mtambo wa kusafisha maji, ujenzi wa bomba kuu la maji kutoka Tumbaku hadi Kingolwira, upanuzi wa mtandao wa kusambaza maji, ukarabati wa miundombinu ya majisafi na ukarabati wa mabwawa ya majitaka. Gharama ya utekelezaji wa mradi huo ni Euro milioni 70. Aidha, kwa sasa Serikali inaendelea na taratibu za kusaini mkataba wa kifedha.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO aliuliza:-
Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuanzisha miradi ya maji mikubwa na midogo na mingine imekabidhiwa kwa wananchi lakini haitoi maji.
Je, Serikali inaweza kueleza ni miradi ipi ya maji mikubwa na midogo iliyokamilika na isiyokamilika katika Mkoa wa Ruvuma na Wilaya zake zote?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naomba Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sikudhani Yassini Chikambo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Ruvuma una jumla ya Halmashauri nane ambapo katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza na ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji Serikali imetekeleza miradi katika vijiji 230 kwa Mkoa wote wa Ruvuma ambapo miradi katika vijiji 94 imekamilika na inatoa huduma ya maji. Miradi mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji katika Halmashauri zote za mkoa huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2017/2018, Mkoa wa Ruvuma umetengewa kiasi cha shilingi bilioni 18.44 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi, ukarabati, usanifu, usimamizi na ufuatiliaji wa miradi ya maji.
Aidha, Serikali itaendelea kutatua tatizo la maji safi na salama kwa kutenga fedha kwa ajili ya kuibua miradi mipya kwa kubaini vyanzo vya maji na kujenga miundombinu ya maji katika Wilaya zote za Mkoa wa Ruvuma sambamba na mikoa mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa maji mijini, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetekeleza miradi ya uboreshaji wa huduma ya maji katika Miji ya Songea, Namtumbo, Mbinga na Tunduru. Hadi kufikia mwezi Machi, 2018 miradi hiyo imekamilika kwa wastani wa asilimia 97 na imegharimu kiasi cha shilingi bilioni 2.6. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Bwawa la Matwiga Wilayani Chunya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa, Mbunge wa Jimbo la Lupa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia programu ya maendeleo ya sekta ya maji ilipanga kutekeleza mradi wa bwawa la Matwiga kwa awamu mbili. Katika awamu ya kwanza Serikali imekamilisha ujenzi wa bwawa la Matwiga lenye uwezo wa kuhifadhi maji mita za ujazo 248,000 kwa ajili ya kuhudumia vijiji 16 vya Matwiga, Isangawana, Mazimbo, Mtanila, Igagwe, Kalangali, Lupa, Ifumwe, Lyeselo, Nkung’ung’u, Majengo, Magungu, Lualaje, Mwinji, Mamba na Mtande. Ujenzi wa bwawa hilo ulianza tarehe 17 Mei, 2015 kwa kwa kumtumia Wakala wa Uchimbaji Visima na Ujenzi wa Bwawa (DDCA) ambapo ulikamilika tarehe 23 Desemba, 2017. Hivi sasa mradi huu uko katika kipindi cha mwaka mmoja wa matazamio (Defect Liability Period).
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mvua nyingi zilizonyesha katika kipindi hiki ambapo bwawa lipo katika muda wa matazamio, kumetokea uharibifu kwenye baadhi ya miundombinu ya utoro wa maji (spillway) ambapo mkandarasi ameagizwa kufanya marekebisho na kuyakamilisha mara baada ya mvua za masika kusisima.
Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya pili ya utekelezaji wa ujenzi wa Bwawa wa Matwiga inahusu ujenzi wa miundombinu ya kutoa maji kwenye bwawa hili kufikisha huduma ya maji kwenye vijiji vilivyokusudiwa. Tathmini ya kumpata mtaalam mshauri wa kusanifu miundombinu ya usambazaji wa maji inaendelea na usanifu wa miundombinu unatarajia kukamilika mwishoni mwa mwezi Julai, 2018. (Makofi)
MASHIMBA M. NDAKI aliuliza:-
Mabonde ya mpunga katika Vijiji vya Masela, Bukangilija na Mwatigi katika Wilaya ya Maswa yanaweza kuzalisha mpunga mwingi kuliko ilivyo hivi sasa.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mabwawa na mifereji ya umwagiliaji katika maeneo hayo ili kuwawezesha wakulima kuongeza tija katika uzalishaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki, Mbunge wa Maswa Magharibi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ina mikakati ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji nchi nzima ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Maswa imekuwa ikiendekeza scheme za umwagiliaji zinazotumia teknolojia ya kuvuna maji ya mvua kwa kujenga mabanio ya kuchepusha maji na mfumo wa mifereji ya umwagiliaji katika mashamba. Kwa maeneo ambayo yemeonekana yanafaa usanifu wa kina hufanyika na kisha ujenzi wa mabwawa ya kuhifadhi maji kwa ajili ya umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Wilaya ya Maswa ipo miradi mbalimbali ya umwagiliai inayotumia mifumo mbalimbali ikiwemo miradi ya umwagiliaji ya Masela, Bukangilija na Mwatigi. Kwa mradi wa Masela wenye eno la hekta 450 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji ulifanywa usanifu wa mwanzo wa ujenzi wa mabwawa na mifereji. Kwa sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina ili ujenzi wa bwawa na mifereji ufanyike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa umwagiliaji wa Bukangilija wenye hekta 307 ulijengwa mwaka 2004 kupitia Mpango wa Kuendeleza Kilimo Wilayani (DADPS) hivyo miundombinu yake imechaka na inahitaji ukarabati mkubwa. Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya ukaratabati wa mradi huo kwa upande wa bonde la Mwatigi lenye ukubwa wa hekari Mwaka 2013 chini ya ufadhili wa World Food Program ulichimbwa mfereji mkuu lakini miundombinu mingine haikujengwa hivyo fedha zitahitajika kukamilisha ujenzi wa mradi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji itaendelea kufanya usanifu wa awali ili kuangalia uwezekano wa ujenzi wa mabwawa katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo maeneo yaliyotajwa. (Makofi)
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA aliuliza:-
Mkoa wa Morogoro umechaguliwa kuwa ni Ghala la Chakula la Taifa hususani katika mazao ya mpunga na miwa. Katika kutaekeleza hili Serikali imepanga kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ujenzi wa skimu za umwagiliaji katika Vijiji/Kata za Usangule – Mto Lwasesa, Igawa – Mto Furua, Lupunga – Mto Mwalisi na Kilosa – Mto Mwalisi.
• Je, ni lini kazi hiyo ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina itakamilika?
• Katika kipindi hiki cha maandalizi ya ujenzi wa mabanio haya ya kilimo cha umwagiliaji, je, Serikali ina utaratibu gani wa usimamizi wa ardhi husika ili kuepuka migogoro ya watumiaji wa mabanio hayo siku za usoni?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa maji na umwagiliaji naomba kijibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda, Mbunge wa Malinyi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Serikali imepanga kufanya upembuzi yakinifu na usanifu kwa ajili ya kuongeza wigo wa kilimo cha umwagiliaji katika maeneo mengi hapa nchini yakiwemo maeneo yaliyotajwa. Utekelezaji wa shughuli hizo unategemea upatikanaji wa fedha. Katika mwaka huu wa fedha 2017 Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imepanga kukamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika Vijiji/Kata za Usengule Mto Lwasesa, Igawa Mto Puma, Lupunga Mto Mwalisi na Kilosa Mto Mwalisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa lengo la kuepuka migogoro ya watumiaji wa mabanio ya maji kwa siku za usoni, Halmashauri ya Malinyi inashauriwa kuandaamipango ya matumizi bora ya ardhi ambapo ardhi inayofaha kwa matumizi ya kilimo cha umwagiliaji itabainishwa na kutengwa rasmi kwa matumizi hayo. Mipango hii itawezesha usimamizi wa kisheria wa ardhi inayofaa kwa umwagiliaji katika maeneo ya vijiji hivyo. Aidha, wakati wa kuanza ujenzi wa mabanio hayo kutaundwa vyama vya umwagiliaji kulingana na sheria ya umwagiliaji ya mwaka 2013. Vyama hivyo vitakuwa na jukumu la kusimamia maeneo hayo na uendeshaji wa skimu za umwagiliaji katika maeneo hayo.
MHE. MAHMOUD H. MGIMWA aliuliza:-
Mheshimiwa Mizengo Pinda akiwa Waziri Mkuu mwaka 2013 aliahidi kuchangia shilingi 295,000,000 katika mradi wa umwagiliaji uliopo kijiji cha Nundwe, kata ya Ihalimba.
Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ili wananchi wa eneo hilo waweze kujikwamua kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mahmoud Hassan Mgimwa, Mbunge wa Mufindi Kaskazini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 2013 alitoa ahadi ya kuchangia kiasi cha shilingi 295,000,000 katika ujenzi wa mradi wa umwagiliaji wa kijiji cha Nundwe kata ya Ihalimba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari serikali ilishaanza utekelezaji wa mradi huo kwa kuwezesha upimaji wa ulalo wa ardhi, usanifu wa banio, ujenzi wa banio, ujenzi wa mfereji mkuu wenye urefu wa mita 2000 na ujenzi wa maumbo ya mashambani. Kazi zote hizo zilikamilika mwaka 2015 na kugharimu kiasi cha shilingi 101,000,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa mradi huo kwa wananchi wa Kijiji cha Nundwe na Taifa kwa ujumla Serikali itaendelea kutafuta na kutoa fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji iliyobaki kwa lengo la kuongeza uhakika wa usalama wa chakula na kipato na hivyo kujikwamua kiuchumi.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza:-
Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alipotembelea Itigi alitoa ahadi ya kusaidia mradi wa maji katika Mji wa Itigi:-
Je, Serikali imetekeleza kwa kiasi gani ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeanza utekelezaji wa mradi wa maji katika Mji wa Itigi ambao ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete. Mradi huu utahusisha Vijiji saba (7) vya Itigi - Mjini, Mlowa, Zinginali, Majengo, Tambuka-reli, Kihanju na Songambele. Kazi zilizofanyika hadi sasa ni utafiti wa vyanzo vya maji yaani (hydrogeological investigation) pamoja na uchimbaji wa visima saba.
Mheshimiwa Spika, kati ya visima saba (7) vilivyochimbwa visima vinne (4) vilipata maji ya kutosha kwa kiasi cha mita za ujazo 3,048 kwa siku ikilinganishwa na mahitaji ya sasa ya mita za ujazo 1,248 kwa siku. Aidha, kazi ya usanifu wa miundombinu ya maji itakayojengwa umekamilika katika Vijiji sita vya Mlowa, Zinginali, Songambele, Tambukareli, Itigi Mjini na Majengo. Kwa upande wa Kijiji cha Kihanju usanifu huo unaendelea. Taratibu za kumpata Mkandarasi wa kujenga miundombinu katika vijiji sita (6) zitaanza hivi karibuni.
Mheshimiwa Spika, mradi huu utatekelezwa kwa awamu tatu; Awamu ya kwanza inahusisha utafiti wa vyanzo vya maji na uchimbaji wa visima ambayo imekamilika. Awamu ya pili inahusisha usanifu wa msambazaji wa maji ambapo umekamilika katika vijiji sita na uandaaji wa makabrasha ya zabuni na manunuzi ya wakandarasi wa ujenzi. Awamu ya tatu itahusisha ujenzi wa miundombinu ya maji.
Mheshimiwa Spika, kukamilika kwa mradi huu kunatarajiwa kuboresha hali ya upatikanaji wa maji kutoka asilimia 47 ya sasa kufikia asilimia 85 kwa wakazi wa Mji huo, pia itawezesha kuanzishwa Mamlaka ya Maji ya Mji wa Itigi.
MHE. JOSEPHINE T. CHAGULA aliuliza:-
Kumekuwepo na tatizo kubwa la ukosefu wa maji safi na salama katika Mkoa wa Geita pamoja na Wilaya zake kama Bukombe, Chato, Mbogwe na Nyang’hwale.
Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza tatizo hilo la maji kwa wananchi wa Mkoa wa Geita na Wilaya zake?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Tabitha Chagula, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma ya maji katika Mkoa wa Geita kwa kutekeleza miradi mbalimbali. Kwa upande wa maji vijijini Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji kupitia Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP II) kwa Halmashauri zote za Mkoa wa Geita kama ilivyo katika Halmashauri zote hapa nchini. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2018 Serikali imetekeleza miradi 66 katika vijiji 217 vilivyopo katika wilaya za Mkoa wa Geita zikiwemo Wilaya za Bukombe, Chato, Mbogwe na Nang’hwale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa maji mijini, Serikali imeendelea na juhudi mbalimbali za kuboresha huduma ya maji ambapo imekamilisha upanuzi wa mtandao wa usambazaji maji na jumla ya kilometa 101.3 za mabomba zimelazwa. Mradi huo umewanufaisha wakazi 14,300 wa Mji wa Geita. Kwa upande wa Mji wa Ushirombo katika Wilaya ya Bukombe, Serikali imekamilisha usanifu wa uboreshaji wa huduma ya maji ambapo mradi huo unawanufaisha wakazi 10,722. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2018, taratibu za kumpata mkandarasi wa mradi huo zinaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Awamu ya Pili ya Utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali kwa lengo la kuwapatia wananchi wengi zaidi huduma ya maji safi na salama.
MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y. MHE. LUCY S. MAGERELI) aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Kimbiji na Mpera chini ya Kampuni ya Serengeti Limited ulianza Machi, 2013 na Desemba 2016 ulitarajiwa kukamilisha visima 20 ambavyo vitawahudumia wananchi wa Kigamboni na Mkuranga. Waziri wa Maji na Umwagiliaji Oktoba, 2016 akitembelea mradi huo na kuagiza ukamilike kwa wakati uliopangwa vinginevyo kampuni ingelipa gharama za ucheleweshaji lakini hadi leo mradi huo haujakamilika:-
(a) Je, Serikali imeshawajibisha kampuni hiyo kwa kuchelewesha utekelezaji wa mradi huo?
(b) Je, ni lini mradi huo utakamilika ili kuondoa adha kwa wananchi wa Kigamboni ambao wengi wao wanatumia maji ya visima vifupi ambavyo sio salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako kabla sijamjibu ndugu yangu, naomba nitoe shukrani za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kusikia kilio cha Waheshimiwa Wabunge kuhusu suala zima la utekelezaji wa miradi vijijini na ameagiza Wahandisi wote waje katika Wizara ya Maji. Nataka niwaambie Wahandisi wa Maji wanyooke na asiyekubali kunyooka basi tupo tayari kumnyoosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mradi wa Uchimbaji wa Visima vya Maji vya Kimbiji na Mpera umechelewa kutekelezwa. Serikali imechukua hatua za kimkataba dhidi ya kampuni husika ikiwa ni pamoja na kukata malipo kwa ucheleweshaji wa kazi (liquidated damage). Mradi wa visima vya Kimbiji na Mpera ilikuwa ukamilike Mei, 2018 sasa unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, maji ya visima hivyo yataanza kutumika baada ya kukamilika kwa awamu ya pili ambayo itahusu ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji ambao utaanza kutekelezwa katika bajeti ya mwaka 2018/2019. Kwa sasa ili kuondoa adha ya wananchi wa Kigamboni wakati wanasubiri kukamilika kwa mradi mkubwa wa Kimbiji na Mpera, Serikali imeanza kutekeleza miradi mbalimbali minne ya uboreshaji wa huduma ya maji kwa mpango wa muda mfupi kwa wakazi wa Kigamboni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hiyo ni pamoja na:-
• Ujenzi wa mtandao wa mabomba ya kusambaza maji kutoka Ruvu Chini kupitia bomba linalovuka bahari eneo la Kurasini kwenda Kigamboni ili kusambaza maeneo ya Tipper, Chuo cha Mwalimu Nyerere na Kigamboni Ferry kuelekea Mjimwema;
• Mradi wa kuendeleza kisima cha Gezaulole ambacho maji yake yatasambazwa Gezaulole na maeneo ya jirani kuelekea Mjimwema;
• Mradi wa ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji kutoka visima vya Vijibweni kuelekea maeneo ya ofisi mpya ya Manispaa ya Kigamboni; na
• Kuendeleza kisima kirefu cha mita 600 cha Kisarawe II ili kufikisha maji Kibada na maeneo ya viwanda (light industry zone) la Kimbiji. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA (K.n.y. MHE. HAROON M. PIRMOHAMED) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza kujenga Skimu za Umwagiliaji za Ipatagwa, Kongoro/ Mswiswi, Motombaya na ujenzi wa Skimu mpya ya Mhwela mpaka Kilambo pamoja na ujenzi wa Banio la Igumbilo, Kata ya Chimala ambalo lilibomolewa na maji mwaka 2016?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haroon Mulla Pirmohamed, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika Bajeti ya Mwaka 2014/2015 ilitekeleza ujenzi wa Skimu za Umwagiliaji za Ipatagwa, Kongoro/ Mswiswi na Motombaya kwa kukarabati mabanio, kuboresha mifereji mikuu na miundombinu ya mashambani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2017/2018, Serikali kupitia Halmashauri ya Mbarali ilitumia kiasi cha shilingi milioni 20 kufanya ukarabati mdogo wa Banio la Igumbilo lililopo katika Kata ya Chimala ili kuwawezesha wakulima kuendelea kutumia banio hilo kwa shughuli za kilimo cha umwagiliaji kwa muda. Ukarabati huu umesaidia na kufanikisha kilimo cha mpunga na mazao mengine kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutafuta fedha kupitia vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa skimu mpya za umwagiliaji katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Skimu ya Mhwela mpaka Kilambo. Aidha, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuweza kukamilisha na kuanza ujenzi wa skimu mpya za umwagiliaji.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa miundombinu ya maji katika Kata za Igowele, Nyololo, Mninga, Mtambula, Nyigo na Idunda?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Igowele, Nyololo, Mninga, Mtambula na Idunda zina jumla ya vijiji 23 vyenye wakazi takribani 69,119. Katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi imetenga shilingi bilioni 2.67 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji vijijini zikiwemo kata hizo. Hadi kufikia sasa usanifu wa kina umekamilika na kwa sasa uandaaji wa makabrasha ya zabuni unaendelea na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Mei, 2018. Kazi hizo zinatekelezwa na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Iringa (IRUWASA) kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu ya miradi hiyo ya maji unatarajiwa kuanza katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, ambapo Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.29 kwa ajili ya miradi ya maji vijijini katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi zikiwemo Kata za Igowele, Nyololo, Mninga, Mtambula, Nyigo na Idunda. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. GODFREY W. MGIMWA aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Kalenga – Tanangozi ni wa muda mrefu na miundombinu yake imechakaa kabisa na hivyo kushindwa kukidhi mahitaji ya wananchi:-
Je, ni lini Serikali itaanza kurekebisha mradi huu ili wananchi wapate maji ya uhakika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji wa Kalenga
– Tanangozi ni mradi uliojengwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na Shirika la Kimataifa la Denmark (DANIDA) na kukamilika mwaka 1982. Mradi huo ni wa maji ya mtiririko ambao ulikuwa unahudumia vijiji 10 vyenye wakazi 12,000 kwa wakati huo. Aidha, kutokana na ongezeko la watu, taasisi mbalimbali na uchakavu wa miundombinu, maji ya mradi huo kwa sasa hayatoshelezi mahitaji ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua adha ya maji ambayo wananchi wanaipata kutokana na kutotosheleza kwa maji katika mradi wa Kalenga – Tanangozi, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika mwaka wa fedha 2017 imeweka mradi huo katika mpango wa ukarabati kwa kutumia fedha za Payment By Result (PBR). Ukarabati utahusisha sehemu zote korofi za mradi huo na hivyo kuwapunguzia adha ya maji wananchi wa Kalenga – Tanangozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa muda mrefu, Serikali inaendelea kutafuta raslimali fedha za kutosha ili kukarabati mradi huo kwa kuwasilisha andiko la mradi kwa wadau wa maendeleo.
MHE. OMARI A. KIGODA - (K.n.y. MHE. OMARI M. KIGUA) aliuliza:-
Wilaya ya Kilindi ni miongoni mwa Wilaya chache zinazopata mvua nyingi nyakati za mvua lakini maji hayo yamekuwa yakipotea:-
• Je, Serikali ipo tayari kuweka utaratibu wa kuvuna maji hayo kwa kujenga mabwawa makubwa ya kuhifadhia maji hayo kwa matumizi ya binadamu?
• Je, Serikali imejipangaje kujenga mabwawa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na ufugaji wa samaki?
NAIBU WAZIRI MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Jimbo la Kilindi, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Wilaya ya Kilindi ni miongoni mwa wilaya zinazopata mvua nyingi hasa mvua za vuli. Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi inaendelea kujenga mabwawa ya kuhifadhi maji ambapo hadi sasa mabwawa matatu (3) katika vijiji vya Saunyi, Jungu na Kwinji/Muungano yamekamilika na hatua inayofuata ni kujenga miundombinu ya maji. Bwawa moja la Mafuleta miundombinu yake imekamilika na linatoa huduma ya maji. Aidha, Serikali itaendelea na ujenzi wa mabwawa na miundombinu yake katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kuvuna maji ya mvua.
• Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, inaendelea kukamilisha mapitio ya Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa Mwaka 2002 ambapo masuala ya ujenzi wa mabwawa yamepewa kipaumbele. Mapitio haya yatabainisha maeneo mbalimbali yanayofaa kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa ya umwagiliaji kwa lengo la kukifanya kilimo cha umwagiliaji kuwa endelevu. Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019, itaendelea kutenga na kutoa fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu wa maeneo yanayofaa kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa ya kuhifadhi maji kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo kilimo cha umwagiliaji.
MHE. JULIUS K. LAIZER aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya ukarabati wa mabwawa matatu katika Kata ya Esilalei ambayo aliahidi tangu mwaka 2015?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2016/2017 ilikamilisha usanifu kwa ajili ya ukarabati wa mabwawa ya Joshoni na Olkuro yaliyopo Halmashauri ya Monduli na kubaini kuwa shilingi bilioni 1.45 zinahitajika kwa ajili ya kazi hiyo. Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya Halmashauri ya Monduli kutekeleza miradi ya maji vijijini ikiwemo ukarabati wa mabwawa hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji katika vijiji vya Lendikinya, Kata ya Sepeko ambao unatekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 868. Kazi imefanyika asilimia 75 na inatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba 2018 kwa kuzingatia mkataba. Aidha, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imeidhinisha shilingi milioni 639 kwa ajili ya ujenzi wa Mradi wa Maji katika Kijiji cha Nanja ambacho kipo Kata ya Lepurko ambako utahudumia pia Shule ya Sekondari ya Nanja, Kata ya Sepeko. Ahsante sana.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO (K.n.y MHE. DKT. DAMAS NDUMBARO) aliuliza:-
Wananchi wa Kata ya Matogoro na Kata ya Seedfarm wanaidai Serikali fidia inayotokana na Serikali kutwaa ardhi yao katika Bonde la Mto Ruhira na mpaka sasa bado hawajalipwa fidia ili wapate ardhi mbadala:-
(a) Je, ni lini Serikali itawalipa wananchi hao fidia stahiki?
(b) Je, Serikali ipo tayari kulipa riba inayotokana na ucheleweshaji wa kulipa fidia ya ardhi kwa wananchi hao?
NAIBU WA WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Damas Daniel, Mbunge wa Songea Mjini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wananchi 803 ambao walikuwa ndani ya mita 60 kutoka kwenye chanzo cha Mto Ruhira walipisha maeneo yao ambapo maeneo hayo kwa sasa yanatumika kama chanzo cha maji kwa wananchi wa Manispaa ya Songea.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015 Serikali kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Songea ilifanya tathmini ambapo jumla ya kiasi cha Sh.1,477,475,000 zilihitajika kwa ajili kulipa fidia kwa wananchi hao. Mwaka 2018 Serikali ilifanya mapitio ya tathmini ya fidia hiyo ili kuendana na thamani halisi ambapo kwa sasa fidia hiyo imefikia kiasi cha Sh.1,913,832,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inakamilisha taratibu za kulipa fidia hiyo kwa kulipa shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2017/2018 na kiasi kilichobakia kitalipwa katika mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. DUA W. NKURUA (K.n.y. MHE. RASHID A. AKBAR) aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuliendeleza Bonde la Mto Ruvuma ili lilete tija kwa wananchi hasa wakulima?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ajali Akbar, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bonde la Mto Ruvuma liko Kusini mwa Tanzania na linapatikana katika Halmashauri za Wilaya za Songea, Namtumbo, Tunduru, Nanyumbu, Newala, Tandahimba na Mtwara. Bonde hilo lina zaidi ya skimu 75 ambazo zinatumika katika kilimo cha umwagiliaji. Serikali kwa kushirikiana na Vyama vya Umwagiliaji imeendelea kuboresha skimu hizo ili kuhakikisha skimu hizo zinaendelea kufanya kazi kama ilivyotarajiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mapitio ya Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa mwaka 2002, maeneo mbalimbali yalibainishwa ikiwa ni pamoja na Bonde la Ruvuma na kuandaliwa mpango mkakati wa uendelezaji wa skimu zilizopo na kuanzisha skimu mpya. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kutekeleza mpango kabambe wa Taifa hususan katika Bonde la Mto Ruvuma.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA (K.n.y. MHE. HALIMA J. MDEE) aliuliza:-
Baadhi ya maeneo katika Jimbo la Kawe yanakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa maji safi na salama kwa kipindi kirefu. Maeneo kama Kata ya Mabwepande (Mtaa wa Mbojo, Mabwepande, Kinondo); Kata ya Makongo (Mtaa wa Changanyikeni na baadhi ya maeneo ya Mtaa wa Makongo Juu); Kata ya Wazo, Mbweni na Mbezi Juu na changamoto hii sugu ilitarajiwa kupungua na kumalizika kabisa baada ya mradi mkubwa wa maji wa Ruvu Chini kukamilika ambao kwa sasa tayari umeshakamilika.
• Je, mikakati ya usambazaji maji pamoja na mabomba katika maeneo ambayo hayana mtandao wa mabomba ikoje ili kutatua kero husika?
• Je, ni miradi gani inayotarajiwa kutekelezwa, muda wa utekelezaji, gharama za kila mradi na nani anayewajibika katika utekelezaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Jimbo la Kawe, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wananchi wa Dar es Salaam hususan maeneo ambayo hayakuwa na mtandao wanaondokana na kero ya kutopata huduma ya maji, Serikali katika awamu ya kwanza kupitia DAWASA inakamilisha ujenzi wa matanki na mabomba makuu ya kupeleka maji katika maeneo ya miinuko ya Changanyikeni, Wazo na Salasala. Aidha, awamu hii pia itahusu ujenzi wa mtandao wa maji Kata ya Kiluvya na Mbezi Luisi. Mradi huu unatekelezwa chini ya ufadhili wa mkopo wa masharti nafuu kutoka India kwa gharama ya dola za Kimarekani milioni 32.772. Hadi sasa utekelezaji wa awamu ya kwanza umefikia asilimia 82 na unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, awamu ya pili ya utekelezaji itahusu ujenzi wa mabomba madogo madogo ya kusambaza maji na kuunganisha wateja katika maeneo yote kuanzia Changanyikeni, Bunju hadi Bagamoyo. Ujenzi wa mradi huu unatarajiwa kuanzia mwezi Julai, 2018 na unatekelezwa chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia kwa gharama ya dola za Marekani milioni 45. Mradi huu utatekelezwa kwa miezi 15. Zabuni ya ujenzi wa mradi huo itatangazwa hivi karibuni baada ya kupata kibali kutoka Benki ya Dunia.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-
Visima virefu vimechimbwa katika Vijiji vya Lugunga na Kabanga (Mkweni) na maji yakapatikana lakini shughuli za ulazaji mabomba na ukamilishaji imekwama. Je, Serikali iko tayari kutoa utaalam na fedha kukamilisha miradi hii?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Mbogwe hadi sasa ina jumla ya watu 137,636 na asilimia 65 wanapata huduma ya maji safi na salama kupitia miradi ya maji minne ya skimu ya usambazaji maji, visima virefu 20, visima vifupi 460 na matanki 55 ya kuvuna maji ya mvua.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe inategemea kujenga miradi ya maji miwili katika Vijiji vitano ambavyo ni Lugunga, Luhala, Kabanga, Nhomolwa na Nyanhwiga. Mradi mmoja wa Kabanga – Nhomolwa na Nyanhwiga ni kutoka chanzo cha kisima kirefu cha Kabanga nan mradi wa pili ni Lugunga – Luhala ni kutoka chanzo cha kisima kirefu cha Lugunga na utahudumia Vijiji vya Luganga na Luhala.
Mheshimiwa Spika, usanifu wa Mradi wa Kabanga – Nhomolwa umekamilika na uko katika hatua ya manunuzi ili kumpata mkandarasi wa ujenzi wa mradi huu. Aidha, miradi wa Lugunga – Luhala bado upo kwenye Halmashauri ya Mbogwe na imetengewa shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya kuanzia ujenzi wa miundombinu ya miradi hii.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu iko tayari kutoa wataalam ili kutatua changamoto za utekelezaji wa miradi hii kulingana na mahitaji.
MHE. SILAFU J. MAUFI aliuliza:-
Kumekuwa na changamoto katika kuwapatia maji safi na salama wananchi wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma pamoja na kuwa Ziwa Tanganyika na Ziwa Rukwa yako katika mikoa hiyo.
Je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kuanzisha mradi wa maji kutoka kwenye vyanzo hivyo na kusambaza kwa wananchi wetu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silafu Jumbe Maufi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kuboresha huduma ya maji kwa wananchi, Serikali imeanza kutekeleza miradi ya kutoa maji katika maziwa makuu nchini kupeleka kwa wananchi wanaozunguka maziwa hayo. Katika Mkoa wa Kigoma, Serikali inatekeleza mradi unaogharimu kiasi cha shilingi bilioni 42 kutoka Ziwa Tanganyika kwenda katika Manispaa ya Kigoma Ujiji ambapo utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2018.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea na jitihada za kutumia vyanzo vya maji vya Ziwa Tanganyika na Ziwa Rukwa kwa ajili ya kuhudumia wananchi wa Mikoa ya Katavi, Rukwa na Kigoma. Hivyo, Wizara imeziagiza Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira za mikoa husika kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa miradi ya maji na uandaaji wa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya miradi ya maji itakayotumia vyanzo hivyo. Utekelezaji wa miradi hiyo ni kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji Awamu ya Pili (WSDP II).
MHE. AZZA H. HAMAD aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kupeleka maji katika Sekondari ya Masengwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Azza Hillal Hamad, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kutekeleza ahadi yake ya kupeleka maji kwenye Shule ya Sekondari Masengwa. Serikali imeandaa mradi wa kutoa maji Kijiji cha Bugweto Manispaa ya Shinyanga kwenda katika Kijiji cha Masengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tararibu za kumpata Mkandarasi atakayetekeleza mradi wa kupeleka maji katika Kijiji cha Masengwa zimekamilika. Utekelezaji wa mradi huo utaanza katika mwaka wa fedha 2018/2019. Matarajio ni kwamba mradi huu utakapokamilika utawanufaisha wakazi wa Kijiji cha Masengwa ikiwemo na Shule ya Sekondari Masengwa.
MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Kutokana na tatizo kubwa la ukosefu wa maji katika Mji Mdogo wa Muze Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ilipitisha mpango wake wa kuondokana na tatizo hilo kwa kuanzisha mradi mkubwa wa kuchukua maji toka Mto Kalumbaleza na kusambaza katika Vijiji vya Muze, Mlia, Mnazi Mmoja Asilia, Ilanga, Mbwilo Kalakala, Isangwa na Uzia:- Je, ni lini Serikali itatoa fedha ili kutekeleza mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Jimbo la Kwela, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutenga fedha za utekelezaji wa miradi ya maji ili kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma ya maji. Kwa sasa Mtaalam Mshauri anaendelea na kazi ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa mradi wa maji wa Muze Group ili utekelezaji wake uweze kufanyika katika mwaka wa fedha 2018/2019.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga kiasi cha Sh.500,000,000 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Muze Group.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-
Tatizo la maji katika Jimbo la Wanging’ombe limekuwa sugu kwa sasa:-
Je, ni lini Serikali itatatua tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kubabiliana na tatizo la maji katika Jimbo la Wanging’ombe ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018, Halmashauri ya Wanging’ombe imetengewa jumla ya shilingi bilioni 4.7 na mpaka Machi, 2018, Serikali imepeleka jumla ya shilingi bilioni Kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji na Usafi wa Mazingira, Halmashauri ya Wanging’ombe imekamilisha miradi katika Vijiji vya Wangama, Mtama, Masaulwa, Isimike, Igenge na Idenyimembe na wananchi wanapata huduma ya maji. Miradi mingine katika vijiji tisa ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Mheshimiwa Spika, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali kupitia fedha za mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Exim ya India itatekeleza mradi wa kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji katika maeneo yanayopata huduma ya maji kutoka mradi wa kitaifa wa Wanging’ombe pamoja na Mji wa Igwachanya. Kazi zinazotarajiwa kutekelezwa ni pamoja na ukarabati wa chanzo cha Mbukwa na Mtitafu; ulazaji wa bomba kuu katika chanzo cha Mbukwa umbali wa kilomita 112; ukarabati wa matanki 59; kulaza bomba kuu kutoka chanzo cha Mtitafu umbali wa kilimita 15; ujenzi wa tanki la ujazo wa lita 200,000 katika eneo la Igwachanya; na ulazaji wa mabomba ya kusambaza maji. Utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kuanza mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. HALIMA ABDALLAH BULEMBO aliuliza:-
Mkoa wa Kagera upo karibu na Ziwa Victoria lakini una uhaba mkubwa wa Maji:-
Je, ni kwa nini Wizara isibuni mradi mkubwa wa kutoa Maji Ziwa Victoria kupeleka Kagera kama ule wa kutoa Maji Ziwa Victoria kwenda Tabora?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima Abdallah Bulembo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mkoa wa Kagera ni miongoni mwa mikoa inayopakana na Ziwa Victoria hapa nchini. Kwa Mkoa wa Kagera, Serikali inaendelea kutumia ziwa hilo, ambapo imekamilisha mradi wa maji Manispaa ya Bukoba na maeneo ya pembezoni yanayozunguka Manispaa hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutatua tatizo la maji katika Mkoa wa Kagera hususan katika Miji ya Kayanga, Omurushaka, Kyaka, Bunazi, Ngara, Muleba na Biharamulo, Serikali inaendelea na taratibu za kumpata Mataalam Mshauri atakayefanya upembuzi yakinifu usanifu wa kina na kuandaa makabrasha ya zabuni ambapo usanifu huo utabainisha jinsi ya kutatua matatizo ya maji kwa Mkoa wa Kagera.
Mheshimiwa Mwenyekti, ushauri wa kutumia Ziwa Victoria kuwa chanzo cha maji katika Mkoa wa Kagera kama ulivyotolewa na Mheshimiwa Mbunge umepokelewa na Mtaalam Mshauri anayetarajiwa kupatikana mwezi huu wa Septemba, 2018 ataangalia uwezekano kuzingatia ushauri uliotolewa.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Novemba, 2016 Serikali ilivunja mabanio (vizibo) vya maji katika Mto Katuma, Mto Mpanda na Mto Mafunsi ambayo yalikuwa yanasaidia wakulima wa zao la mpunga na mengineyo katika Mkoa wa Katavi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mabanio (vizibo)ili matumizi ya maji yawe haki kwa kila kiumbe kama sheria hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji; naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji Na. 11 ya mwaka 2009 kifungu namba 43 kinamtaka mtu yeyote anayetaka kuchepusha au kuchukua maji kutoka chanzo chochote cha maji ikiwemo mito, maziwa, mabwawa au maji chini ya ardhi lazima awe na kibali na awe kibali cha kutumia maji kutoka Bodi ya Maji ya Bonde husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Novemba, 2016 Serikali ilivunja miundombinu ya umwagiliaji (mabanio) iliyopo katika Mito ya Katuma, Mpanda na Mifunsi kutokana na miundombinu hiyo kujengwa bila kuwa na vibali vya kutumia maji kama sheria inavyoelekeza, hivyo kusababisha Mbuga ya Katavi na Vijiji ambavyo viko chini kukosa maji. Mwezi Agosti, 2017 Wizara kupitia Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Rukwa kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mpanda iliainisha maeneo nane yanayofaa kujengwa miundombinu ya umwagiliaji katika Mito ya Katuma, Mpanda na Mafunsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2018/2019 Serikali ilitenga shilingi bilioni 2.750 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo katika Mito ya Katuma, Mpanda na Mafunsi.
MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mradi wa umwagiliaji wa Mkoga Irrigation Scheme uliopo katika Manispaa ya Iringa Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ernest Kabati, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imeendelea kutekeleza ujenzi wa scheme mbalimbali hapa nchini. Katika mwaka wa fedha 2014/2015 Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kupitia mfuko wa Food Aid Counter Party ilitumia kiasi cha shilingi milioni 270 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya mashambani na ujenzi wa mfereji mkuu katika scheme ya umwagiliaji ya Mkoga yaani Mkoga Irrigation Scheme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu wa scheme hiyo haujakamilika na bado unahitaji kiasi cha shilingi bilioni 2.1 kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya umwagiliaji mashambani. Hivyo Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imeingiza scheme ya umwagiliaji ya Mkoga kwenye awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango kabambe wa Taifa wa umwagiliaji utakaoanza kutekelezwa kuanzia mwaka wa fedha 2018/2019 hadi mwaka 2025/2026.
MHE. DAVID E. SILINDE aliuliza:-
Tatizo la maji Wilaya ya Momba halijapatiwa ufumbuzi wa kudumu mpaka sasa.
Je, ni lini Serikali ya Awamu ya Tano itamaliza tatizo hilo katika Wilaya ya Momba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI aliuliza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua tatizo la maji katika Wilaya ya Momba katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya Programu ya Maendeleo ya Maji yaani WSDP, Serikali imekamilisha ujenzi wa miradi sita katika Vijiji vya Namtambalala, Iyendwe, Itumbula, Mnyuzi, Chilulumo na Kamsamba katika Jimbo la Momba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu ya Pili ya Utekelezaji ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, jumla ya vijiji 10 vimependekezwa ili kuendelea kuboresha huduma ya maji katika Halmashauri ya Momba. Vijiji vilivyopendekezwa ni pamoja na Vijiji vya Ikana, Namsinde, Nkangamo, Mpapa, Chole, Itelefya, Chitete, Tindingoma, Kasinde na Samang’ombe. Serikali itaendelea kutatua tatizo la majisafi na salama kwa kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya kubaini vyanzo vipya vya maji na kujenga miundombinu ya maji katika Halmashauri ya Momba kwa kadri fedha zitakavyopatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali imechimba visima virefu viwili katika vijiji vya Chitete na Tindingoma. Usanifu wa miradi hiyo miwili upo katika hatua za mwisho za kutangaza zabuni kwa ajili ya kuwapata wakandarasi wa ujenzi. Uchimbaji wa kisima kingine katika kijiji cha Ikan
MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-
Mheshimiwa Rais Mstaafu, Dkt. Jakaya Kikwete alipokuwa kwenye harakati za Uchaguzi Mkuu mwaka 2005 alikubali kuwa mlezi wa Shule ya Sekondari Mahenge na akaahidi kutatua tatizo sugu la maji katika shule hiyo.
Je, ni lini Serikali itaipatia shule hiyo maji safi na salama kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais Mstaafu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua tatizo la maji safi na salama linalozikabili baadhi ya shule za sekondari hapa nchini, ikiwa ni pamoja na Shule ya Sekondari Mahenge iliyoko Wilayani Kibiti. Ili kukabilina na tatizo hilo katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 36 kwa ajili ya miradi mbalimbali ya elimu sekondari wilayani humo. Kati ya hizo fedha shilingi milioni 10 zitatumika kwa ajili ya mradi wa maji safi na salama katika Shule ya Sekondari Mahenge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga na kutoa fedha za miradi ya maji katika maeneo mbalimbali ikiwemo maeneo ya shule.
MHE. ESTER A. BULAYA aliuliza:-
Kilimo cha umwagiliaji katika Mji wa Bunda kimekuwa kikitengewa fedha kidogo sana kiasi cha kutokidhi mahitaji kazi husika.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuiwezesha Ofisi ya Umwagiliaji ya Wilaya ili kufanya kilimo kuwa cha kisasa, endelevu na chenye kuleta tija kwa wananchi wa Bunda?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Amosi Bulaya, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya miradi ya umwagiliaji ili kuboresha kilimo cha umwagiliaji katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Bunda. Katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo (ASDP I), Serikali ilijenga mabwawa mawili ya Maliwanda na Kisagwa na kujenga skimu tatu za umwagiliaji zenye hekta 220,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutafuta fedha kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa skimu katika Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Bunda. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuendelea kuboresha kilimo cha umwagiliaji ili kiweze kuleta tija na kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na malighafi kwa ajili ya viwanda.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Je, Serikali inajua tatizo la ukosefu wa maji Kilolo linasababishwa na nini na nini suluhisho lake?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Jimbo la Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji, imeandaa mipango madhubuti katika kuhakikisha inaboresha huduma ya maji kwa wananchi wa Mji wa Kilolo. Katika lengo hilo Wizara inatekeleza mpango wa muda mfupi na muda mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa muda mfupi, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la USAID kupitia programu ya WARIDI, inatekeleza kazi za uboreshaji wa huduma ya maji kwa Mji wa Kilolo. Kazi zinazotekelezwa katika mradi huo ni ukarabati wa kitekeo cha maji (chanzo cha maji), ujenzi wa bomba kuu lenye urefu wa kilometa 12.8, ujenzi wa mtandao wa usambazaji maji wenye urefu kwa kilometa sita, ujenzi wa vituo sita vya kuchotea maji, ujenzi wa tanki lenye ujazo wa mita za ujazo 100 na ukarabati wa matanki matatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Machi 2018, utekelezaji wa mradi huo umekamilika kwa wastani wa asilimia 90. Kukamilika kwa mradi huo kutawanufaisha wakazi 6,200 wa Mji wa Kilolo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali imakamilisha usanifu wa mradi wa maji katika Mji wa Kilolo. Kazi zitakazotekelezwa ni ujenzi wa chanzo cha maji katika Mto Mtitu, ujenzi wa mtambo wa kuchuja maji, ujenzi wa bomba kuu, ujenzi wa mtandao wa usambazaji maji na ujenzi wa mfumo wa umeme wa kuendesha mitambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi huo utakapokamilika utaongeza uzalishaji wa maji kutoka lita 380,000 kwa siku hadi lita milioni 4.4 kwa siku ifikapo mwaka 2025, ambapo mahitaji ya maji kwa sasa ni lita milioni 2.7 kwa siku. Gharama za utekelezaji wa mradi huo ni dola za Marekani milioni 4.3. Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
MHE. LUCY S. MAGERELI (K.n.y. MHE. MWITA M. WAITARA) aliuliza:-
Jimbo la Ukonga katika Kata za Msongola, Chanika, Zingiziwa, Buyuni na Pugu kuna shida kubwa sana ya maji.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa muda mrefu wa kuondoa kero ya maji katika kata hizo?
(b) Je, ni lini miradi viporo vya maji na visima vyenye pampu mbovu vitafanyiwa matengenezo ili kupunguza kero ya maji Ukonga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikabe Waitara Mbunge wa Jimbo la Ukonga lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango wa muda mrefu wa kuondoa kero ya maji katika Jiji la Dar es Salam na viunga vyake kwa kutumia maji ya visima virefu 20 vilivyochimbwa katika Manispaa ya Kigamboni eneo la Kimbiji na Mpera vyenye uwezo wa kutoa kiasi cha maji cha mita za ujazo 350 mpaka 700 kila kimoja. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya kusafirisha na kusambaza maji katika maeneo hayo. Kukamilika kwa mradi huu kutaondoa kero ya maji katika Jiji la Dar es Salam na viunga vyake zikiwemo Kata za Msongola, Chanika, Zingiziwa Buyuni na Pugu. Mradi huu unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2018/2019.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu ya Pili ya Utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP II) Serikali imeweka kipaumbele cha kukamilisha miradi viporo kabla ya kuanza miradi mingine mipya. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imepanga kukamilisha miradi viporo na kukarabati visima vyenye pampu mbovu kwa kutumia fedha za Mpango wa Malipo kwa Matokeo (Payment by Result). Mpaka sasa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala imekarabati na kumalizia ujenzi wa miradi viporo sita ya maji katika Jimbo la Ukonga kwenye Kata za Msongola, Pugu, Mzinga na Pugu Stesheni.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatatua tatizo la maji katika Jimbo la Njombe Kusini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Awamu ya Pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji inaendelea kutekeleza miradi ya maji katika Halmashauri zote nchini, ambapo kwa mwaka wa fedha 2017/2018, Halmashauri ya Njombe imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 1.55 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi na ukarabati wa miradi ya maji. Mpaka sasa Serikali imekamilisha Miradi ya Maji katika Vijiji vya Peruhanda, Limage, Igominyi, Igoma na Iwongilo. Miradi mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuboresha huduma ya maji Njombe Mjini ambapo ni Makao Makuu ya Mkoa mpya wa Njombe, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali inatekeleza mradi kutoka Chemchem ya Kibena kwa gharama ya shilingi bilioni 1.1. Hadi kufikia Mei, 2018, kazi zilizokamilika ni ulazaji wa bomba kuu lenye urefu wa kilomita 2.2; ujenzi wa kidakio cha maji; ununuzi wa dira za maji na ufungaji wa pampu mbili za kusukuma maji zenye uwezo wa kuzalisha maji mita za ujazo 72 kwa saa. Kwa ujumla utekelezaji wa mradi umefikia asilimai 90 na unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali itatekeleza mradi wa maji kutoka Mto wa Hagafilo kwa ajili ya kutoa huduma ya maji kwa wakazi wa Njombe Mjini na maeneo ya pembezoni mwa mji huo. Usanifu wa mradi huo umekamilika na kazi zitakazotekelezwa ni ukarabati wa chanzo cha Magoda; ujenzi wa chanzo cha Mto Hagafilo; ulazaji wa bomba kuu; ulazaji wa mabomba ya usambazaji; ujenzi wa matanki na ufungaji wa dira za maji. Mradi huo utagharimu Dola za Marekani milioni 13.5 ikiwa ni mkopo nafuu kutoka Serikali ya India. (Makofi)
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Je, Serikali itakamilisha lini mradi wa kusambaza maji kwa wananchi waliopo pembezoni mwa bomba kuu litokalo Ruvu Juu hadi Dar es Salaam hususan wananchi wa Kata za Kwembe, Mbezi, Kibamba, Msigani na Saranga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Msuha, Mbunge wa Mbinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imemwajiri mkandarasi Kampuni ya Jain Irrigation Services kutekeleza mradi wa usambazaji maji kwa wananchi waishio maeneo ya pembezoni mwa bomba kuu litokalo Ruvu Juu hadi Dar Salaam hususani wananchi wa Kata za Kwembe, Mbezi, Msigani na Saranga.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Mei, 2018, utekelezaji wa mradi huo ulikuwa umekamilika kwa wastani wa asilimia 87. Kazi inayoendelea kwa sasa ni kukamilisha ulazaji wa mabomba na kufanya majaribio (Pressure test). Mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2018. (Makofi)
MHE. MARY P. CHATANDA - (K.n.y MHE. STEPHEN H. NGONYANI) aliuliza:-
Serikali ilitenga shilingi bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la Mkomazi lakini baadaye Serikali ilihamishia fedha hizo mkoa mwingine:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha fedha hizo ili bwawa lililokusudiwa lijengwe?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, awali ya yote, naomba nimpe pole Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wake wa Korogwe Vijijini kwa msiba wa kufiwa na mke wake kipenzi. Mwenyezi Mungu ailaze mahali pema peponi roho ya marehemu.
Mheshimiwa Spika, lakini kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stephen Hillary Ngonyani Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kati ya mwaka 2003 na 2004 wananchi wa Kijiji cha Manga Mikocheni, Kata ya Mkomazi, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe walionesha hitaji la mradi wa kuendeleza kilimo cha umwagiliaji kwa zao la mpunga katika Bonde la Mkomazi. Aidha, kwa mwaka wa fedha wa 2006/2007, Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa wakati huo kupitia Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Kilimanjaro ilifanya upembuzi yakinifu na usanifu wa awali ambapo walibaini kuwa jumla ya shilingi bilioni 13 zingehitajika kuendeleza bonde la Mkomazi ikiwemo ujenzi wa bwawa hilo.
Mheshimiwa Spika, aidha, upembuzi huo, ulibainisha kuwa ujenzi wa bwawa hili ungesababisha Ziwa Manga lilipopo katika Kijiji cha Manga ambalo lina maji ya chumvi kuchanganya maji yake ya Bwawa la Mkomazi hivyo maji yote kuwa ya chumvi ambayo yangeathiri kilimo cha zao la mpunga.
Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto hii mwaka 2014/2015, Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Kilimanjaro ilifanya mapitio ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kuepuka kuzamisha Ziwa Manga na kubaini kuwa jumla ya shilingi bilioni 1.5 zingehitajika kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hilo.
Mheshimiwa Spika, katika kufikia azma hiyo, Serikali kupitia bajeti ya mwaka 2015/2016, ilitenga jumla ya shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa Bwawa la Mkomazi. Hata hivyo, fedha za ndani zilizotengwa kwa ajili ya mradi huo hazikupatikana na hivyo kusababisha mradi huo kutotekelezwa.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa mradi huo na hasa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Wizara kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji inatarajia kuliingiza bwawa hilo katika vipaumbele vya kutekeleza Mpango Kabambe wa Umwagiliaji wa Taifa ambao kwa sasa unafanyiwa mapitio kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA). Mapitio hayo yanatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, 2018. (Makofi)
MHE. EDWARD F. MWALONGO - (K.n.y. MHE. DEO K. SANGA) aliuliza:-
Mji wa Makambako unakabiliwa na tatizo kubwa la maji kutokana na ongezeko la watu na Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni aliahidi kuanza kwa ujenzi wa mradi wa maji na kazi ya usanifu wa mradi huo imeshafanyika:-
Je, ni lini sasa ujenzi wa mradi huo wa maji utaanza?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Mkambako, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia awamu ya kwanza ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP I) imekamisha upembuzi yakinifu na usanifu wa mradi wa kuboresha huduma ya maji katika Mji wa Makambako. Kazi zitakazotekelezwa katika mradi huo ni pamoja na ujenzi wa Bwawa Tagamenda, uchimbaji wa visima virefu vya Idofi na chemichemi ya Bwawani, ujenzi wa bomba kuu na mfumo wa usambazaji wa maji na matanki makubwa ya kuhifadhi maji. Mradi huo unatarajiwa kunufaisha wananchi wapatao 155,253.
Mheshimiwa Spika, Serikali imepata fedha za kutekeleza mradi huo kupitia mkopo wa masharti nafuu kutoka Serikali ya India wa Dola za Marekani milioni 500 zitakazotumika kutekeleza miradi ya maji katika Miji mbalimbali ukiwemo Mji wa Makambako. Tayari Serikali imesaini Mkataba wa Kifedha na Serikali ya India na ujenzi wa mradi huo unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. SAED A. KUBENEA (K.n.y. MHE. JOSEPH R. SELASINI) aliuliza:-
Vipo vyanzo vya maji kutoka Mlima Kilimanjaro ambavyo vinasemekana vinapeleka maji nchini Kenya kupitia msitu wa Rongai:-
Je, Serikali haioni sababu za kudhibiti vyanzo hivyo ili kuhakikisha kwamba maji hayo yanatumika katika Halmashauri ya Rombo badala ya kwenda nchi jirani ya Kenya?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Raman Selasini, Mbunge wa Rombo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ipo miradi ya maji kwa upande wa Kenya inayotumia vyanzo vya maji vilivyopo katika msitu wa Rongai ambapo kuna mito na chemchem 14 inayopeleka maji Loitokitok nchini Kenya. Maji hayo yanachukuliwa kwa vibali vya Bonde la Mto Pangani. Kijiografia wananchi wa Loitokitok hawana sehemu nyingine jirani ambayo wangeweza kupata maji. Upelekaji wa maji Mji wa Loitokitok ni wa kihistoria.
Mheshimiwa Naibu Spika, ufuatiliaji uliofanywa na wataalam wa Wizara kwa kushirikiana na wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo umebaini kuwa maji hayo yalianza kuchukuliwa tangu miaka 1960 ambapo ipo miradi ya maji yenye vibali vya mwaka 1960, 1990, 2000 na baada ya 2010. Baada ya ufuatiliaji huo, watumiaji wote wametakiwa kuomba vibali upya kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji Na.11 ya 2009. Maji yanayochukuliwa ni kutoka kwenye vyanzo vidogo ambavyo haviwezi kutumika katika mji mdogo wa Tarakea.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na vyanzo hivi kuwa na maji kidogo, kuna uwezekano wa kuchepusha ili kuwasaidia wananchi wetu wa mpakani hasa maeneo ambapo mabomba yanapita ili kudumisha ujirani mwema wa pande zote mbili. Kwa sasa Kampuni ya Kiliwater ambayo ndiyo inayotoa huduma ya majisafi Wilayani Rombo imeomba kibali cha kuchukua maji kutoka Mto Naremuru na tayari kibali cha ujenzi kwenye chanzo hicho kimepatikana.
MHE. AISHAROSE N. MATEMBE aliuliza:-
Uhaba wa maji safi na salama imekuwa ni kero kubwa kwa wananchi wa Wilaya ya Manyoni na Mkoa wa Singida:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuanzisha miradi mikubwa ya maji ambayo itahudumia wananchi wa maeneo hayo muda wote?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aisharose Ndogholi Matembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ya maji kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji na katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Programu jumla ya miradi minne ya Solya, Kilimatinde, Londoni na Majiri imekamilika na wananchi wanapata huduma ya maji. Katika awamu ya pili ya utekelezaji wa Programu, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni inatekeleza miradi ya Mangoli, Itetema, Kasanii, Kintinku, Maweni, Makuru, Nyaranga, Makutupora, Sanza/Ntope, Makanda, Igwamadete, Heka, Chikombo na Mazuchi ambayo ipo katika hatua za utafutaji wa vyanzo na kufanya usanifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, upo mradi mkubwa wa Mbwasa ambao umeshafanyiwa usanifu na utaanza kutekelezwa katika mwaka 2018/2019 kwa ajili ya kuhudumia vijiji vya Mbwasa, Mwiboo, Chikuyu, Mtiwe, Chilejeho, Mvumi, Ngaiti, Kintinku na Lusilile.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2018/2019, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni imetengewa jumla ya shilingi bilioni 1.3 na Serikali itahakikisha miradi hiyo inatekelezwa na inakamilika mapema na kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa maeneo hayo.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-
(a) Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi zake ikiwemo ya Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni za kutoa maji Mto Zigi kwenda Muheza na Vijiji vyake?
(b) Je, Serikali ina mpango gani zaidi ya huo wa kuwaletea maji wananchi wa Muheza?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba na Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza kutekeleza ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambapo imekamilisha usanifu wa kutoa maji kutoka Mto Zigi kwenda Mji wa Muheza.
Mheshimiwa Spika, kazi zitakazotekelezwa katika mradi huo ni ujenzi wa kitekeo cha maji (Intake) katika Mto Zigi, ujenzi wa mtambo wa kutibu maji, ulazaji wa bomba kuu lenye urefu wa kilometa 23, uunganishaji wa vijiji vitakavyopitiwa na bomba kuu umbali wa kilometa 12 kila upande, pamoja na upanuzi na ukarabati wa mtandao wa usambazaji maji katika Mji wa Muheza.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/ 2018, Serikali imeendelea na utekelezaji wa oboreshaji wa huduma ya maji katika Mji wa Muheza, kwa mpango wa muda mfupi. Kazi zinazotekelezwa ni ulazaji wa mabomba urefu wa kilomita 16.9 kutoka Pongwe Jijini Tanga hadi Kitisa Wilaya ya Muheza. Gharama za utekelezaji wa mradi huo nishilingi milioni 413.5
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, Serikali imetenga kiasi cha fedha shilingi bilioni 3.17 kwa ajili ya kuendelea na uboreshaji wa huduma ya maji katika Mji wa Muheza na vijiji mbalimbali katika Wilaya hiyo.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Upatikanaji wa maji safi na salama katika Mji wa Kasulu bado ni changamoto kubwa sana, kwani maji yanayotoka kwenye mabomba ni machafu.
Je, ni lini Serikali itatoa pesa kwa ajili ya kununua chujio la maji ili wananchi waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua tatizo la maji katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu ikiwa ni pamoja na miradi ya maji kutokuwa na miundombinu ya kutibu maji katika bajeti ya mwaka 2017/2018. Kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, Halmashauri ya Mji wa Kasulu imetengewa shilingi bilioni 3.35 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya maji ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya kusafisha na kutibu maji. Hadi sasa usanifu wa miradi minne ya Muganza, Marumba, Muhunga na Kimobwa katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu umekamilika na taratibu za kuwapata Wakandarasi watakaotekeleza ujenzi wa miradi hiyo zinaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya kutibu maji ni sehemu ya mradi wa maji wa Kimobwa ambao utaambaatana na uchimbaji wa visima virefu vitano, usambazaji wa bomba la kilometa 14, ujenzi wa tenki lenye ukubwa wa mita za ujazo 225 na ukarabati wa vyanzo vitatu vya maji kwa ajili ya eneo la mji wa Kasulu.
Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu ya kutibu na kusafisha maji itasaidia kuondoa kero ya ubora duni wa maji yanayotumika hivi sasa hususan maji yanayotoka katika vyanzo vya maji vya Miseno, Nyanka, Nyankatoke na Mto Chai. Hivyo ubora wa maji, uzalishaji na usambaji wa maji kwa pamoja utaongezeka. Lengo ni kuhakikisha maji yanayosambazwa kwa wananchi ni safi, salama na yanayokidhi mahitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, zabuni kwa ajili ya kazi hiyo imetangazwa tarehe 24 Machi, 2018 na utekelezaji wake utaanza mara tu baada ya mikataba ya ujenzi kusainiwa.
MHE. AZZA H. HAMAD aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Bwawa la Umwagiliaji katika Kijiji cha Ishololo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Azza Hillal Hamad, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mradi wa ujenzi wa Bwawa la Ishololo uliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini ni moja kati ya miradi iliyokuwa ikitekelezwa kupitia Mradi wa Uwekezaji katika Kilimo chini ya iliyokuwa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika. Utekelezaji wa mradi huo ulifikia ukomo wake mwezi Desemba, 2013 ambapo Benki ya Afrika ilisitisha kutoa fedha za utekelezaji wa mradi wakati utekelezaji wake ulikuwa bado haujakamilika.
Mheshimiwa Spika, Serikali ina dhamira ya dhati ya kukamilisha skimu zote za umwagiliaji ambazo utekelezaji wake haujakamilika kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ukosefu wa fedha. Kwa sasa Serikali inakamilisha mapitio ya Mpango kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa mwaka 2002 ambao unabainisha hali ya skimu za umwagiliaji nchini.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia umuhimu wa kilimo cha umwagiliaji nchini Serikali itatoa kipaumbele kwa miradi yote itakayobainishwa ukiwemo mradi wa umwagiliaji katika Kijiji cha Ishololo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.
MHE. QAMBALO W. QULWI aliuliza:-
Eneo la Mang’ola katika bonde la Eyasi, Wilayani Karatu ni maarufu sana kwa kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia chemchem za Qangded. Chemichemi hizo ziko katika hatari ya kutoweka kutokana na kuingiliwa na shughuli za kibinadamu:-
Je, ni lini Serikali itaweka mpango madhubuti wa uhifadhi wa chemchem hizo ikiwa ni pamoja na kuweka mipaka kwa kutumia sheria zilizopo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Qambalo Willy Qulwi, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupitia Bodi ya Maji ya Bonde la Kati kwa kushirikiana na wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu na Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, mwaka 2017 ilifanya tathmini ya uharibifu wa mazingira, matumizi ya maji na mipaka ya chanzo hicho ambapo yafuatayo yalibainika:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo cha Qang’dend kimehifadhiwa kwa kuwekewa mpaka tangu mwaka 2006 na baadaye mwaka 2014 kwa umbali wa kuanzia mita 145 hadi mita 595 kulingana na eneo lilivyo katika maeneo yenye chemchem na umbali wa kuanzia mita 84 hadi mita 303 kwa baadhi ya maeneo ya kandokando ya Mto Mang’ola ambayo chanzo chake ni chemchem ya Qang’dend. Alama za mipaka zilizosimikwa haziheshimiki na wananchi katika baadhi ya maeneo kutokana na kwamba zingine zimejificha chini ya ardhi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, pili, pampu zote za umwagiliaji zimeondolewa kwenye mto na kuwekewa nje ya mto kwenye umbali ambao hazina athari kwenye chanzo. Pia tathmini imebaini kuwa tatizo la chemchem kukauka limechangiwa na mchanga ama udongo mwingi uliosafirishwa kutoka maeneo ya juu ya chemchem na mito midogo iliyoingiza maji katika mto Mang’ola ambapo imesababisha kuziba kwa macho ya chemchem hizo.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, tatu; hatua zilizopangwa kutekelezwa na Wizara yangu ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi juu ya utunzaji wa vyanzo, kuweka mipaka madhubuti katika maeneo yote muhimu ya chanzo na kuondoa michanga iliyoziba chemchem hiyo.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-
Wilaya ya Mkalama iliyoko Mkoani Singida hupata mvua chini ya wastani na maji yote ya mvua hutiririka na kupotea.
i. Je, Serikali inachukua hatua zipi kutoa kipaumbele kwa Wilaya ya Mkalama kujengewa mabwawa makubwa hasa ikizingatiwa kuwa fedha za ndani (own sorce) za Halmashauri haziwezi kutosheleza ujenzi wa huduma hii?
ii. Je, ni lini Serikali itafanya utafiti kuona kiwango cha maji kinachopotea wakati wa mvua na kutoa ushauri wenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji imeziagiza Halmashauri zote nchini kuainisha maeneo yanayoweza kujengwa mabwawa na kutenga fedha kwenye bajeti zao kwa ajili kujenga angalau bwawa moja kwa mwaka. Katika mwaka 2017/2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama imeendelea na kazi ya kuainisha maeneo kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa ambapo hadi sasa Vijiji vya Kitumbili, Nkito, Malaja, Nkalankala, Lyelembo na Nduguti kazi hii imekamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti wa maji hufanyika linapofanyika zoezi la kuyatambua maeneo yanayofaa kujengwa mabwawa ili kujua kiasi cha maji kinachoweza kuhifadhiwa katika mabwawa hayo ikilinganishwa na mahitaji. Hivyo, kazi hii ya utafiti ya maji yanayopotea kipindi cha mvua yanaweza kufanyika sambamba na zoezi la kuainisha maeneo yanayofaa kwa kujengwa mabwawa. (Makofi)
MHE. PHILIPO A. MULUGO aliuliza:-
(a) Je, ni nini mpango wa Serikali kuhusu Ziwa Rukwa hasa kwa kuzingatia kudumaa na kukosekana zao la samaki katika Ziwa hilo?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuliendeleza bonde la Ziwa Rukwa hasa katika kilimo cha umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Philipo Augustino Mulugo, Mbunge wa Songwe, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa shughuli za uvuvi katika Ziwa Rukwa hudumaa na kukosekana kwa zao la samaki. Hali hii ilkuwa ikisababishwa na changamoto mbalimbali kubwa ikiwa ni uvuvi haramu ambapo wavuvi hutumia dhana haramu za uvuvi ambazo ni makokoro na nyavu zisozoruhusiwa kuvua. Pia uchafuzi wa mazingira unaotokana na kuongezeka kwa shughuli za binadamu kama vile uchimbaji wa madini na shughuli za kilimo karibu na Ziwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri zinazozunguka Bonde la Ziwa Rukwa imeweka utaratibu unaozingatia sheria ambapo shughuli za uvuvi kwa baadhi ya maeneo hufungwa ili kuwapa nafasi samaki kukua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Bonde la Ziwa Rukwa linafaa kwa shughuli za kilimo cha umwagiliaji kutokana na kuwa na mito mingi yenye kutiririsha maji mwaka mzima na maeneo yanayofaa kwa kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uwepo wa fursa hizo katika bonde hilo Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imeendelea kuboresha kilimo cha umwagiliaji kupitia Skimu za Ifumbo, Mshewe na Utengule, Bara, Ipunga, Iyura na Mbulumlowo, Naming’ongo, Sakalilo na Ng’ongo, Kilida, Mwamkulu, Kakese, Uruila na Usense.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji itaendelea kuboresha skimu zote za umwagiliaji zilizopo kwenye Bonde la Ziwa Rukwa na hivi sasa Serikali imeliweka Bonde la Ziwa Rukwa kwenye mpango ulioboreshwa na kuendeleza kilimo cha umwagiliaji Kitaifa.
MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:-

Mradi wa maji toka Ziwa Victoria utapeleka maji kwenye Wilaya za Busega, Bariadi na Itilima kwa awamu ya kwanza.

Je, kwa nini Serikali isipeleke maji hayo Makao Makuu ya Wilaya zote za Mkoa wa Simiyu katika awamu ya kwanza ili kutatua shida ya maji inayojitokeza mara kwa mara katika miji hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mradi huu umepangwa kutekelezwa kwa awamu mbili kutokana na upatikanaji wa fedha. Fedha kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya kwanza kwa ajili ya miji ya Wilaya ya Busega, Bariadi, Itilima pamoja na vijiji 170 zimepatikana. Awamu hiyo itagharimu kiasi ya Euro milioni 105 ambapo Benki ya KfW ya ujerumani itatoa Euro milioni 25 na Green Climate Fund itatoa Euro milioni 80.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa awamu ya pili utahusisha miji ya Mwanhuzi na Maswa pamoja na vijiji vipatavyo 83. Kwa sasa Serikali inaendelea na majadiliano na Green Climate Fund kwa ajili ya kupata fedha kiasi ya Euro milioni 208 kwa ajili ya utekelezaji awamu hii.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa awamu ya pili unatarajiwa kuanza baada ya kukamilisha taratibu za upatikanaji wa fedha. Serikali itaendelea na juhudi za kuhakikisha fedha kwa ajili ya utekelezaji awamu hii zinapatikana mapema ili kuwezesha wananchi wa Mkoa wa Simiyu kupata huduma ya maji kama ilivyotarajiwa.
MHE. SUZANA C. MGONUKULIMA aliuliza:-

Je, Serikali inasema nini kuhusu Mradi wa Maji kutoka Ibofye kwenda Magulilwa, Kuhota, Lyamgun’we, Ifunda ambao ulipitishiwa bajeti na Bunge?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonukulima, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo:-


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 1982, kupitia ufadhili wa DANIDA, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa ilifanya upembuzi yakinifu wa Mradi wa Maji wa Mtitiriko (Gravity Scheme) utakaotumia chanzo cha maji cha Mto Mtitu ili kuweza kuhudumia vijiji 34 vilivyopo katika Kata sita za Magulilwa, Kuhota, Mseke, Ifunda, Mgama na Maboga ambazo zilikuwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kabla ya kugawanyika na kuundwa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo. Mradi huo ulikadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi milioni 596.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya utekelezaji wa mradi huo kuanza kuligundulika chanzo kingine cha Mto Ibofye katika Kijiji cha Ihimbo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ambacho kingeweza kutumika kwa ufanisi zaidi na kutatua tatizo la maji kwa kata hizo. Hata hivyo, usanifu wa mradi huu haukukamilika na unategemewa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2019/2020. Mradi huu unatarajiwa kuhudumiwa vijiji 17 na kati ya hivyo vijiji 15 vipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa na vijiji viwili katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo wanapata huduma ya maji wakati wakisubiri Mradi wa Ibofye, Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa pamoja na wadau wa maendeleo ilichimba visima 53 ambavyo vimewezesha wakazi 8,200 wa kata hizo kupata huduma ya maji. Aidha, ukarabati wa visima katika Kata za Ifunda na Mgama umekamilika na tayari vinatoa huduma kwa wananchi.
MHE. JULIUS K. LAIZER aliuliza:-

Tatizo la maji Jimbo la Monduli limeongeze kwa sasa baada ya Mabwawa zaidi ya 43 kati ya 51 kujaa tope na mengine kupasuka:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa muda mfupi na muda mrefu wa kuwapatia maji wananchi wa Esilalei, Makuyuni, Mswakini na Ohukai kabla ya mwaka 2020?

(b) Mradi wa maji ya kisima cha Ngaramtoni umefika katika Kata ya Monduli Mjini na Engutoto; je, ni lini Serikali itasambaza maji kwa wananchi wa Vijiji vya Lashaine, Ar Katan na Meserani chini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika juhudi za kuwapatia maji wananchi wa Esilalei Makuyuni, Mswakini na Otukai kabla ya mwaka 2020 Serikali imekuwa ikijenga mabwawa ya kuhifadhi maji katika Wilaya ya Monduli kutokana na Wilaya hiyo kukosa vyanzo vya uhakika vya maji kama vile chemchem na vyanzo vya maji chini ya ardhi. Kwa upande wa Vijiji vya Makuyuni na Mswakini vinapata maji kupitia visima virefu vilivyochimbwa kwenye vijiji hivyo na vijiji vya Esilalei na Otukai vinapata maji kupitia vyanzo vya Bwawa ya Otukai, Esilalei na JKT Makuyuni.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017/2018 Serikali ilitekeleza mradi wa maji wa Ngaramtoni ambapo awamu ya kwanza ilihusisha huduma ya usambazaji katika kijiji cha Meserani Juu. Awamu ya pili itahusisha usambazaji wa maji katika Kijiji cha cha Meserani Chini na kazi hiyo inategemea kuanza mwezi Julai, 2019. Kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Monduli imetengewa jumla ya shilingi bilioni
1.2 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji. Serikali itaendelea kutenga fedha na kutoa fedha ili kuhakikisha hadi kufikia mwaka 2020 vijiji vyote vya Arktana, Nanja, Esilalei, Makuyuni, Mswakini, Otukai na Mti Mmoja vimepatiwa huduma ya maji.
MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

Upatikanaji wa maji safi na salama katika Jimbo la Nsimbo ni asilimia 40 chini ya wastani wa kitaifa vijijini wa asilimia 61.1 ili kufikia wastani huo inahitajika fedha kiasi cha bilioni 15:-

Je, Serikali ipo tayari kuitengea Halmashauri ya Nsimbo angalau bilioni tatu kila mwaka wa fedha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Jimbo la Nsimbo, kama ifuatvyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019 imeitengea Halmshauri ya Wilaya ya Nsimbo kisi cha shilingi bilioni 1.413 ikiwa ni fedha kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji inayoendelea kutelezwa katika vijiji vya Sitalike, Igongwe, Itenka, Nduwi pamoja na ufungaji wa pampu za mkono katika vijiji vya Kashelami, Kapanda, Wenyeji, Imilamate, Kambuzi Halt, Ofisi ya DED - Nsimbo, Katambike, Kabuga, Kituo cha Afya Katumba, Buremo, Ikondamoyo na Ndurumo A.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wananchi wote wananufaika na huduma ya maji wakiwemo wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo Serikali imejiwekea lengo la kuhakikisha huduma ya maji inafikia asilimia 85 upande wa maji vijijini na asilimia 95 miji ya mikoa ifikapo 2020. Hivyo, Serikali itaendelea kutenga fedha mwaka hadi mwaka kwa ajili ya utekelezaji wa miradi maji nchi kote ili kuweza kufikia malengo hayo.
MHE. DKT. TULIA ACKSON (K.n.y HAROON M. PIRMOHAMED) aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka maji maeneo katika maeneo ya Kata za Mahongele katika vijiji (6), Kata ya Mwatenga vijiji (4), Kata ya Kongoro/Mswiswi vijiji (2), Kata ya Utengule - Usangu vijiji (6), Kata ya Luhanga vijiji (4), Kata ya Itambo vijiji (4), Kata ya Chimala vijiji (7), Kata ya Ihahi vijiji (3), Kata ya Imalilo – Songwe vijiji (5), Kata ya Igaua vijiji (5), Kata ya Miyombweni vijiji (5), Kata ya Mapogoro vijiji (9) na Mji wa Rujewa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haroon Mulla, Mbunge wa Jimbo Mbarali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kupitia Progamu ya Maji Vijiji tangu mwaka 2012 imefanya usanifu katika vijiji 16 na kujenga miradi ya maji katika vijiji Simike-Kata ya Utengule Usangu, Udindilwa - Kata ya Ruiwa, Igurusi - Kata ya Igurusi, Chimala - Kata ya Chimala, Mkunywa -Kata ya Madibira na Ubaruku - Kata Ubaruku. Pia Halmashauri kupitia kwa wadau wa maelendeleo (UNICEF) imechimba visima 25 katika vijiji mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kukamilisha miradi hiyo, Halmashuri inaendelea na utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa Luduga Mawindi ambao hadi utapokamilika utagharima shilingi bilioni 9 na utahudumia vijiji sita vya Kata ya Mawindi na Ipwani. Mradi huu utatekelezwa kwa awamu tano na kwa sasa utelezaji unaendelea katika awamu ya kwanza ambayo imefikia asilimia 98 na awamu ya pili imefikia asilimia 75. Hadi sasa mradi huu umegharimu shilingi bilioni 2.9. Taratibu za kutangaza awamu ya 3 zinaendelea na awamu ya 4 na 5 zitatangazwa baada awamu ya 3 kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa lengo la kuboresha huduma ya maji katika Mji wa Rujewa mji huo pia umejumuishwa katika miji itakayonufaika kupitia fedha za mkopo kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 500 kutoka Serikali ya India ambazo zitatumika katika ujenzi na ukarabati wa miradi ya maji katika maeneo mbalimbali nchini.
MHE. AMINA S. MOLLEL (K.n.y. MHE. HAWA M. CHAKOMA) aliuliza:-

Kuna miradi mikubwa ya maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha ambayo hadi sasa haijakamilika. Miradi hiyo ipo Kijiji cha Mperamumbi Kata ya Kwala, Kijiji cha Boki Mnemera Kata ya Bokomnemera, Kijiji cha Vukunti Kata ya Mlandizi na Kijiji cha Dutumi Kata ya Dutumi:-

Je, ni lini miradi hiyo itakamilika ili kuwaletea matumaini wananchi wa maeneo hayo, hususan akinamama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2013, Serikali ilianza kutekeleza miradi ya maji mikubwa katika Vijiji vya Mperamumbi, Kata ya Kwala, Boko Mnemela, Kata ya Bokomnemela na Vukunti, Kata ya Mlandizi vilivyopo Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha. Utekelezaji wa miradi hiyo imekamilika mwaka 2018 na tayari inatoa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi. Miradi hii ina changamoto ya uendeshaji inayosababisha maji kukatwa mara kwa mara kutokana na bili ya maji kuwa kubwa. Kwa kuwa eneo la Kibaha linapatiwa maji na DAWASA, Wizara inaangalia uwezekano wa mradi huo kusimamiwa na DAWASA na si Jumuiya ya Watumiaji Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Dutumi umekamilika na unatoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi na kwa sasa mradi huo unafanyiwa upanuzi kutoka vituo sita (6) hadi kufikia vituo tisa (9) vya kuchotea maji.
MHE. AMINA N. MAKILLAGI aliuliza:-

Tatizo la maji linaendelea kuwa kubwa siku hadi siku katika maeneo mbalimbali:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ya majisafi na salama vijijini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassor Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto kubwa ya upatikanaji wa fedha inayokabili ujenzi wa miundombinu ya maji katika maeneo mbalimbali nchini. Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali kupitia programme ya maendeleo ya Sekta ya Maji awamu ya pili iliyoanza mwezi Julai, 2016, imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo kwa kutenga na kutoa fedha za kujenga, kupanua na kukarabati miradi ya maji katika maeneo ya maji Vijijini, Miji Mikuu ya Mikoa, Miji Mikuu ya Wilaya, Miji midogo pamoja na Miji na Vijiji vinavyohudumiwa na miradi ya maji ya Kitaifa. Lengo ni kufikia asilimia 85 ya wananchi wanaopata huduma ya majisafi na salama katika maeneo ya vijijini na asilimia 95 kwa maji mijini ifikapo 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha fedha za ndani zinapatikana za kutosha na kwa wakati kwa ajili ya utekelezaji wa miradi, Serikali imeanzisha Mfuko wa Maji ambao umekuwa chanzo cha uhakika wa fedha kwa ajili ya miradi ya maji hususan vijijini. Kutokana na jitihada hizo za kutafuta fedha za miundombinu ya maji, hadi sasa huduma ya maji vijijini imefikia asilimia 64.8 na kwa upande wa mijini imefikia asilimia 80.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutafuta vyanzo mbalimbali vya fedha ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha miundombinu ya maji inajengwa katika maeneo mbalimbali na kutoa huduma ya maji kwa wananchi.
MHE. DKT. TULIA ACKSON (K.n.y. MHE. SAUL H. AMON) aliuliza:-

Wilaya ya Rungwe ina vyanzo vingi vya maji ambavyo vinatiririsha maji.

Je, ni lini Serikali itarekebisha miundombinu ili kuongeza kiwango cha maji ambayo kwa sasa hayatoshi kiasi cha kufanya Idara ya Maji kufunga baadhi ya maeneo kama vile Vijiji vya Ibungila, Lubiga na kadhalika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saul Henry Amon, Mbunge wa Jimbo la Rungwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe inakadiriwa kuwa na jumla ya wakazi wapatao 291,176. Huduma ya maji imegawanyika katika maeneo makuu mawili; eneo la kwanza ni huduma ya maji Mjini Tukuyu inayotolewa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tukuyu na eneo la pili ni huduma ya maji vijijini inayotolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la mijini, watu wapato zaidi ya 32,074 wanapata huduma ya maji kati ya watu 50,000 sawa na asilimia 63. Katika maeneo ya vijijni, watu wapatao 157,750 wanapata huduma ya maji kati ya watu 240,250 sawa na asilimia 55.7. Vyanzo vya maji vinavyotegemewa na wananchi wa Rungwe ni vijito, mito na chemchemi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Ibungila na Lubiga vilikuwa vinapata huduma ya maji kutoka katika mradi wa maji wa Mji wa Tukuyu, uliojengwa tangu mwaka 1984 ambapo kuanzia mwaka 2002 unasimamiwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tukuyu. Hata hivyo, kutokana na kuongezeka kwa watu na uchakavu wa miundombinu ya usambazaji maji, kwa sasa huduma ya maji katika Vijiji vya Ibungila na Lubiga haipatikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali inaendelea na ukarabati wa miundombinu ya maji katika Mji wa Tukuyu ambao katika mwaka wa fedha 2017/2018 imetoa shilingi milioni 3,087 kupitia Mamlaka ya Maji Mjini Tukuyu ili kuongeza upatikanaji wa maji. Fedha hizo zitafanya kazi ya ujenzi wa tank lenye mita za ujazo 200 na kukarabati mtandao wa bomba kilomita tisa. Utekelezaji wa mradi huo unaendelea. Hadi sasa ujenzi wa tank umekamilika na bomba za inchi sita zenye jumla ya urefu wa mita 750 zimelazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utekelezaji wa mradi huu kukamilika vijiji vya Ibungila na Lubiga vitaweza kupata huduma ya maji kutokana na ukarabati unaoendelea kufanyika hivi sasa.
MHE. KISWAGA B. DESTERY aliuliza:-

Serikali ilikuwa na mpango wa kupeleka maji katika Mji wa Kisesa - Bujora na Kata ya Bukandwe:-

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga na kupeleka maji katika miji hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya na Shirika la Maendeleo la Ufaransa inatekeleza Programu ya Majisafi na Usafi wa Mazingira katika Jiji la Mwanza na Miji ya Magu, Lamadi na Misungwi na miradi ya Majitaka katika Miji ya Bukoba na Musoma kwa gharama ya EURO million 104.5.

Aidha, kupitia programu hii, AFD imeridhia kutoa fedha ya nyongeza (additional financing) kiasi cha EURO milioni 30 sawa na shilingi bilioni 75 kwa masharti ya mkopo nafuu. Kwa sasa mchakato wa kutia saini Mkataba wa Makubaliano ya Kifedha (Financing Agreement) kati ya AFD na Wizara ya Fedha na Mipango unaendelea.

Mheshimiwa Spika, kulingana na andiko la mradi, fedha hizo za nyongeza zitatumika kutekeleza mradi wa kupeleka maji katika maeneo ya Usagara, Buhongwa, Busweru na Mji mdogo wa Kisesa - Bujora na Kata ya Bukandwe pamoja na Vijiji vya Igetimaji, Kitumba, Mwahuli, Busekwa na Ihayabuyaga. Mradi huu unategemewa kuanza katika mwaka wa fedha 2019/2020.

Hivyo, nawaomba wananchi wa Kisesa, Bujora na Kata ya Bukandwe wawe na subira kwa kuwa mpango wa kuwapelekea maji uko katika hatua nzuri.
MHE. DKT. JASMINE T. BUNGA aliuliza:-

Kumekuwepo na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi dhidi ya Mamlaka za Maji Safi katika Halmashauri mbalimbali kwa kuwapatia wananchi bili kubwa za maji ambazo haziendani na uhalisia:-

Je, ni lini Serikali itaanzisha utaratibu wa kulipia maji kadri utumiavyo katika utoaji wa huduma hiyo kama ilivyo kwenye umeme?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Jasmine Tisekwa Bunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza kutumia utaratibu wa kulipa maji kadri unavyotumia (pre-paid meters) katika maeneo mbalimbali nchini. Kwa sasa utaratibu huo umeanza kutumika katika maeneo yanayohudumiwa na Mamlaka za Arusha, Iringa, Songea, Dodoma, Tanga, Mbeya, Tabora, Mwanza, Moshi na DAWASA.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeagiza Mamlaka zote nchini kuendelea kuwafungia wananchi dira za maji za kulipa maji kadri watumiavyo ili kupunguza malalamiko ya wananchi pamoja na kupunguza tatizo la malimbikizo ya madeni ya matumizi ya maji.
MHE. ALLAN J. KIULA aliuliza:-

Pamoja na mambo mengine, Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano imelenga kuongeza asilimia za upatikanaji wa maji vijijini.

(a) Je, lini Serikali itafanya utafiti wa vyanzo vya maji katika Jimbo la Mkalama ili kuwa na uhakika wa rasilimali hiyo?

(b) Je, lini Serikali itatoa fedha za kutosha kuwapatia maji safi wananchi wa Jimbo la Mkalama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Allan Joseph Kiula, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki, lenye kipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, Serikali kupitia Wizara ya Maji imetenga kiasi cha shilingi milioni 450 kwa ajili ya kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi katika maeneo kame ya Mikoa ya Singida, Mwanza, Tabora na Shinyanga. Utafiti huo utahusisha pia Wilaya ya Mkalama ambapo shilingi milioni 50 zitatumia.

Mheshimiwa Spika, pamoja na utafiti unaotarajiwa kufanyika, Serikali imekua ikitekeleza miradi mbalimbali yamaji katika Vijiji vya Ndunguti, Kinyangiri, Ipuli na pia inatekeleza miradi ya uchimbaji wa visima 24 katika maeneo mengine tofauti. Ili kuhakikisha miradi hii inakamilika Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 1.36 kwa mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-

Baada ya Serikali kukamilisha usanifu wa mradi wa maji wa vijiji 57 kwenye kata 15 Wilayani Kyerwa:-

Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha kwenye Bajeti ya 2019/2020 ili miradi hiyo ianze kutekeleza Ilani ya CCM ya kumtua mama ndoo kichwani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mradi wa vijiji 57 kwenye kata 15, Wilayani Kyerwa ni miongoni mwa miradi mikubwa ya maji ambayo Serikali ina mpango wa kuitekeleza ili kuhudumia wananchi wengi. Mradi huu unalenga kuhudumia watu takriban 282,000 waishio kwenye vijiji hivyo utakapokamilika.

Mheshimiwa Spika, usanifu wa mradi huu umekamilika na imeonekana kuhitaji kiasi kikubwa cha fedha. Hivyo, Serikali inafanya jitihada za kutafuta fedha za kutekeleza mradi huu wa kimkakati (Strategic Water Project).
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza:-

Serikali inajitahidi sana kukabiliana na tatizo la maji katika Manispaa ya Morogoro, lakini tatizo hilo lipo kwenye baadhi ya Kata:-

Je, Serikali ina mikakati gani ya makusudi ya kumaliza tatizo hili katika Manispaa ya Morogoro?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA) inaendelea na uboreshaji wa huduma ya maji katika Manispaa ya Morogoro kwa mipango ya muda mfupi na muda mrefu. Katika mipango ya muda mfupi, katika mwaka wa fedha 2018/2019, MORUWASA imetekeleza mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji katika Kata za Kihonda na Mkundi. Mradi huo umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 1.9 na umewanufaisha wakazi wapatao 17,000 wanaoishi maeneo ya Kihonda Kilimanjaro, Yespa, Kiegea na Kihonda Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika la Maendeleo la AFD itatekeleza mradi wa kuboresha huduma ya majisafi katika Manispaa ya Morogoro. Kazi zitakazotekelezwa ni kuongeza kina cha bwawa la Mindu, ujenzi wa mtambo wenye uwezo wa kusafisha na kutibu maji, upanuzi wa mtambo wa kusambaza maji, ukarabati wa mabwawa ya majitaka kwa gharama ya Euro milioni 70. Kwa sasa Wizara inasubiri kusainiwa kwa mkataba wa kifedha kati ya Wizara ya Fedha na Shirika la Maendeleo la Ufaransa la AFD kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
MHE. JOHN J. MNYIKA aliuliza:-

Tarehe 4 Februari Serikali ikijibu hoja binafsi kuhusu upatikanaji wa maji iliahidi kuwa ifikapo mwaka 2016 matatizo ya maji yangekuwa yamemalizika katika Jiji la Dar es Salaam:-

(a) Je, ni kwa nini ahadi hiyo haijatekelezwa kwa wakati?

(b) Je, ni Mitaa ipi katika Jimbo la Kibamba maji hayatoki na ni lini DAWASA itahakikisha maji yanatoka katika maeneo hayo?

(c) Je, Serikali iko tayari kuwasilisha katika kila Mkutano wa Bunge Taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maji nchini kama ilivyokubali katika Bunge la Kumi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Myika, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengi ya Jiji la Dar es Salaam yanapata maji kama Serikali ilivyoahidi kupitia Bunge lako Tukufu baada ya kukamilisha miradi mikubwa ya maji ambayo ilikamilika mwaka 2016. Serikali inatambua kuna baadhi ya maeneo ya jiji hilo hayajapata maji kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ongezeko la watu na ukuaji wa Jiji la Dar es Salaam pamoja na upatikanaji wa maeneo ya kupitisha miundombinu ya miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 80 ya wakazi wa Jimbo la Kibamba wanapata huduma ya maji. Maeneo ambayo hayapati maji kwa sasa ni maeneo ambayo yapo kwenye miinuko mikubwa. Ili kuhakikisha wananchi wote wa Jimbo la Kibamba wanapata maji, hasa wanaoishi katika miinuko mikubwa, Serikali inaendelea na ujenzi wa matenki katika eneo la Msakuzi Kusini na Maramba Mawili Juu kwa lengo la kuhakikisha wananchi wote wa Jimbo hilo wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi Kiti kilishalitolea mwongozo suala hili katika Mkutano wa Pili, Kikao cha Tisa kilichofanyika tarehe 5 Februari, 2016. Katika mwongozo wa Kiti ilielekezwa kama ifuatavyo; naomba kunukuu; “Bunge la Kumi na Moja litakuwa linaweka utaratibu wake wa namna bora kufikisha maelezo kwa Waheshimiwa Wabunge kwa nyakati tofauti.”

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. JEROME D. BWANAUSI (K.n.y. MHE. ENG. RAMO M. MAKANI) aliuliza:-

(a) Je, nini mpango wa Serikali kukamilisha mradi wa maji safi unaoendelea katika Mji wa Tunduru ili kuwaondolea wananchi hao adha kubwa wanayoipata ya uhaba wa huduma hiyo?

(b) Jimbo la Tunduru Kaskazini lina vijiji 92 ambapo taarifa za Serikali na takwimu zinaonesha kiwango cha upatikanaji wa maji kuwa chini sana:-

Je, ni lini mpango wa Serikali wa kuongeza kiwango hicho cha upatikanaji wa maji katika vijiji hivyo kufikia kiwango kilichowekwa kwa mujibu wa mipango ya Serikali na Ilani ya CCM itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ramo Makani, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2016/2017 Mji wa Tunduru ulitengewa fedha kiasi cha shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya maji Mjini Tunduru na kuongeza hali ya upatikanaji wa maji. Uboreshaji huo ulisaidia kuongeza huduma ya maji kutoka asilimia 52 mwaka 2017 kufikia asilimia 66 kwa sasa. Aidha, kwa mwaka huu wa fedha 2018/2019, kupitia mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Songea, inaendelea na utaratibu wa kutekeleza mradi wa upanuzi wa miundombinu ya maji kwa mji wa Tunduru ambapo wananchi wengi zaidi watapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Jimbo la Tunduru Kaskazini lina jumla ya vijiji 92 vyenye vituo vya kuchotea maji 385 vinavyohudumia wakazi wapatao 58,250. Katika kuhakikisha huduma ya maji safi na salama inaongezeka katika vijiji vilivyopo, Jimbo la Tunduru Kaskazini, Serikali inatekeleza miradi miwili ya Nandemo ambao umekamilika na mradi wa Matemanga ambao umefikia asilimia 85 ya utekelezaji na utahudumia vijiji vya Matemanga, Milonde, Changarawe na Jaribuni. Lengo la Serikali ni kuhakikisha huduma ya maji vijijini inafikia asilimia 85 ifikapo mwaka 2020 kama inavyoelekeza Ilani ya CCM.
MHE. BALOZI. DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:-

Mto Kagera ni chanzo muhimu kinachoweza kusaidia upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wanaopakana nao:-

Je, kwanini Serikali isifanye utaratibu wa kuvuta maji hayo ili yawasaidie wakazi wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Diodorus Buberwa Kamala, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshaanza mipango ya kutumia Mto Kagera kama chanzo cha maji katika maeneo mbalimbali yanayopakana na Mto huo. Kwa sasa Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Bukoba (BUWASA) imepanga kuutumia Mto Kagera kama chanzo cha maji kwa Miji ya Kyaka na Bunazi pamoja na vijiji mbalimbali vinavyozungukwa na mto huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji wa mradi kwenda Miji ya Kyaka na Bunazi kwa kutumia chanzo cha mto huo, BUWASA imemwajiri mtaalam mshauri kwa ajili ya kufanya usanifu na uandaaji wa makabrasha ya zabuni na matarajio ya usanifu huo utakamilika mwezi Septemba, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matarajio ya ujenzi wa mradi huo utaanza katika mwaka wa fedha 2020/2021.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-

(a) Je, ni kwa nini Serikali imeshindwa kukamilisha mradi wa visima 23 ambavyo vingesaidia kama suluhisho la muda mfupi la tatizo la maji safi na salama katika Mji wa Tarime hususan kwenye maeneo ya Kata za pembezoni kama Nyandoto (Masurula), Nkende, Ketare, Kenyamanyori, Nyamisangura na Turwa?

(b) Mheshimiwa Rais alipofanya ziara Jimbo la Tarime Mjini Julai, 2018 aliwaeleza wananchi kuwa Serikali imetenga takriban shilingi bilioni 14 kwa ajili ya maji kutoka Ziwa Victoria ambayo itaondoa kabisa tatizo la maji katika Mji wa Tarime. Je, ni hatua gani imefikiwa kwenye ahadi hiyo hasa ikizingatiwa kuwa mradi huo upo kwenye mchakato kwa miaka mingi sasa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicolas Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Musoma (MUWASA) imeingia mkataba na Wakala wa Uchimbaji wa Visima na Ujenzi wa Mabwawa (DDCA) kwa ajili ya uchimbaji wa visima 23 katika Mji wa Tarime kwa gharama ya shilingi milioni 536.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa DDCA wanaendelea na utafiti wa maji chini ya ardhi (hydrological survey) na matarajio ya kazi ya uchimbaji wa visima hivyo itakamilika mwezi Septemba, 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utekelezaji wa ahadi ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa wananchi wa Tarime, Serikali imeshapata fedha kutoka Serikali ya India kiasi cha dola za Marekani milioni 500 kwa ajili ya uboreshaji wa huduma ya maji kwa miji 28 ya Tanzania Bara pamoja na Zanzibar ambapo Mji wa Tarime ni miongoni mwa Miji itakayopata maji kupitia fedha hizo. Kwa sasa taratibu za kuwapata wataalam washauri watakaofanya usanifu wa kina na uandaaji wa makabrasha ya zabuni unaendelea. Matarajio ya ujenzi wa miradi hiyo itaanza katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa maji wa Katoro- Buseresere unaokusudia kutoa maji Ziwa Victoria?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lolesia Jeremia Bukwimba, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kutekeleza miradi ya maji ambayo lengo lake ni kufikisha huduma ya maji kwa asilimia 95 ya wakazi wa mijini na asilimia 85 ya wakazi wa vijijini hadi ifikapo mwaka 2020. Malengo hayo yanahusu pia maeneo ya Katoro na Buseresere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa Majisafi kutoka Ziwa Victoria kwenda Miji ya Katoro na Buseresere ambapo hadi hivi sasa mazungumzo ya awali kati ya Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) na wafadhili kutoka Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB) yamefanyika. EIB wameonesha nia ya kufanya mradi wa maji kwa ajili ya miji hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, andiko ya mradi wa maji kwa ajili ya miji ya Katoro na Buseresere limeshawasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango ili maombi yaweze kuwasilishwa rasmi EIB.
MHE. DKT. MARY M. NAGU aliuliza:-

Maeneo mengi katika Wilaya ya Hanang’ yana matatizo ya maji ingawa Kata za Dirma, Lalaji, Wandela, Gawidu, Bassodesh na Mwanga zina visima vilivyochimbwa licha ya maji kutopatikana:-

Je, Serikali ina mikakati gani ya kutatua matatizo ya maji katika wilaya hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mary Michael Nagu, Mbunge wa Hanang’, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika juhudi za kutatua matatizo ya maji katika Wilaya ya Hanang’, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji katika maeneo mbalimbali ya Wilaya hiyo katika Vijiji vya Hirbadaw, Kata ya Hirbadaw na Murumba, Kata ya Lalaji utekelezaji wa miradi upo katika hatua za mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Vijiji vya Bassodeshi, Nyabati, Gijetamuhog, Murumba, Gorimba, Diloda na Qalosendo katika Kitongoji cha Merekwa wananchi wanapata huduma ya maji kupitia visima vilivyochimbwa. Sehemu ya Kijiji cha Dirma iliyopo Kata ya Dirma inapata maji kutoka kwenye Mradi wa Maji ya Mtiririko wa Nangwa. Kijiji cha Gawidu ni miongoni mwa vijiji vitakavyojumuishwa katika miradi ya Bassotu ambapo utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 90. Aidha, utekelezaji wa mradi huo utaendelea katika vijiji vingine kwa awamu kwa mwaka wa fedha 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali ni kuendelea kutekeleza miradi mipya, kukamilisha inayoendelea na kukarabati ya zamani kwa kadri fedha zitakapopatikana ili kuhakikisha wananchi wa Wilaya ya Hanang’ wanapata huduma ya maji na yenye kutosheleza.
MHE. QAMBALO W. QULWI aliuliza:-

Kijiji cha Makhoromba ni kati ya vijiji 10 vilivyopangwa kunufaika katika mpango wa WSDP-I Wilayani Karatu. Hadi hivi sasa Wilayani Karatu mradi wa maji katika kijiji hicho haujatekelezwa:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza mradi huo ili wananchi hao waondokane na tatizo kubwa la kukosa huduma ya maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Qambalo Willy Qulwi, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Makhoromba kina vitongoji vinne na kwa sasa upo mradi uliotekelezwa na Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro kwa kushirikiana na wananchi pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, ambao unatoa huduma katika vituo vitatu vya kuchotea maji, lakini kutokana na ugumu wa kijiografia haukuweza kufika kila kitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuona umuhimu wa kutatua tatizo la uhaba wa maji katika maeneo mengi ya kijiji hicho, Serikali iliweka kijiji hicho kuwa miongoni mwa vijiji 10 vilivyopangwa kunufaika na programu ya WSDP-I. Aidha, mradi wa maji katika kijiji hicho haukutekelezwa kwa kuwa kipaumbele kiliwekwa katika ukamilishaji wa miradi mingine ya WSDP-I iliyokuwa imeanza kutekelezwa kabla ya kluanzisha miradi mipya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeelekeza Halmashauri ya Wilaya ya Karatu kutafuta vyanzo vya uhakika vyenye maji ya kutosha vitakavyoweza kuhudumia maeneo mengi ya kijiji hicho kulingana na jiografia yake na kufanya usanifu wa mradi huo utengewe fedha katika mwaka wa 2019/2020.
MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y. MHE. SUSAN L. KIWANGA) aliuliza:-

Mji Mdogo wa Mlimba unazungukwa na Kata za Chisano, Kalengakelo na Kamwene na zina jumla ya wakazi wasioupungua elfu hamsini na nane ambapo hawana maji kwa matumizi ya nyumbani na kunywa; na kwa kuwa kuna chanzo kikubwa cha maji na Mhandisi wa Halmashauri ameshaleta andiko la mradi wa maji:-

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za mradi huo ili wananchi hao wapate maji ya kunywa safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto ya maji kutotosheleza wakazi wa Kata za Mlimba, Chisano, Kalengakelo na Kamwene waliopo katika Jimbo la Mlimba, Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero kwa kushirikiana na Wizara ya Maji imesanifu mradi mkubwa wa maji ambao utahudumia wakazi zaidi ya 29,713. Mradi huu utakapokamilika utatatua kero ya maji katika kata zilizotajwa hapo juu ikiwemo Mlimba kwa kuondoa mgao wa maji kabisa.

Andiko la mradi huu linafanyiwa kazi na Wizara ya Maji ili Serikali iweze kutafuta fedha zaidi ya shilingi bilioni 4.5 kuweza kufanikisha ujenzi wa mradi huu ambao umeonekana kuwa suluhisho la maji katika Jimbo la Mlimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika jitihada hizo za kuwapatia wananchi wa Jimbo la Mlimba huduma ya maji safi na salama, Serikali kupitia program ya maji inaendelelea na ujenzi wa mradi wa maji wa Kata za Chita/ Ching’anda a Mbingu/Vigaeni. Pia imekamilisha ujenzi wa miradi ya maji saba katika Vijiji vya Tangamyika, Masagati, Matema, Kamwene, Viwanja Sitini, Mlimba A na B, Namwawala na Idete.
MHE. GIMBI D. MASABA aliuliza:-

Serikali iliahidi kujenga Mradi mkubwa waMaji kutoka Ziwa Victoria kuanzia Nyashimo, Ngasamo, Dutwa, Bariadi, Itilima, Meatu na Maswa:-

Je, ni lini mradi huo utaanza na kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika,kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gimbi Dotto Masaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali itatekeleza mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka katika Miji ya Nyashimo (Busega), Bariadi na Langangabilili, Maswa na Mwanhuzi. Mtaalam Mshauri anaendelea na kazi ya usanifu na uandaaji wa makabrasha ya zabuni na mradi huu utatekelezwa katika awamu mbili.

Mheshimiwa Spika, awamu ya kwanza itahusisha Miji ya Nyashimo (Busega), Bariadi na Lagangabilili pamoja na vijiji vipatavyo 170 vilivyo ndani ya kilomita 12 kutoka bomba kuu kila upande. Awamu hii itagharimu Euro milioni 105 ambapo kati ya hizo Serikali ya Ujerumani kupitia benki yake KfW itatoa Euro milioni 25naGreen Climate Fund(GCF) Euro milioni 80. Ujenzi waawamu ya kwanza unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2019 na kukamilika mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, awamu ya pili ya mradi itahusisha Miji ya Mwanhuzi, Maswa na vijiji vipatavyo 83. Kwa sasa Serikali inaendelea na majadiliano na Green Climate Fund ili kupata fedha kiasi cha Euro milioni 208 zitakazotumika kugharimia utekelezaji wa awamu hii. Ujenzi wa awamu ya pili utaanza baada ya kukamilisha taratibu za upatikanaji wa fedha hizo. Kukamilika kwaawamu zote kutawanufaisha wananchi wapatao 834,204.
MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza:-

Miradi ya maji katika vijiji vya Lupunga, Ruvu Dosa na Kipandege Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha bado inasuasua mpaka sasa.

Je, ni lini miradi hiyo itapatiwa fedha ili iweze kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji Lupunga uliopo Kata ya Kikongo ulianza kutekelezwa Novemba, 2013 na ulikamika mwaka 2016 na unaendelea kutoa huduma ya maji katika vitongoji tisa vya Ngeta, kikongo, Lupunga, Mwanabwito, Makongotopola, Kisabi, Madimula, Msongola na Makazi Mapya kwenye mamlaka ya mji mdogo wa Malandizi. Mradi huo ulikuwa na changamoto za kiundeshaji ambapo kamati ya Maji ya awali ilivunjwa na kuundwa kamati mpya inaendelea kutoa huduma ya maji maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji Ruvu kwa Dosa uliopo katika Kata ya Matambani ulianza kutekeleza mwaka 2013 na kukamilika mwaka 2016 kutoka bomba kuu la DAWASA. Kwa sasa mradi unaendelea kutoa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi 1800 kwa eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Maji kipandege uliopo katika Kata ya Soga ulianza kutekelezwa Novemba, 2013 na kukamilika mwaka 2017. Mradi huo kwa sasa una changamoto za kiufundi ikiwa ni msukumo mdogo wa maji toka bomba la DAWASA. Tayari Mkandarasi na Mhandisi Mshauri aliyesanifu wanashukulikia tatizo hilo. Lengo la Serikali ni kuhakikisha miradi yote inatoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa maeneo hao.
MHE. PETER A. LIJUALIKALI aliuliza:-

Je, kwa nini Serikali isifute kodi kwenye vifaa vya kusambazia maji kutokana na matatizo ya maji tuliyonayo katika Taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Peter Ambrose Lijualikali, Mbunge wa Jimbo la Kilombero, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tarehe 12 Septemba, 2017, Bunge lako Tukufu lilipitisha marekebisho ya Sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani, Sura ya 148. Marekebisho ya Sheria hiyo ya VAT yalihusisha vifungu vya 6 na 7 pamoja na aya ya 9 ya sehemu ya pili ya Jedwali la Sheria ya VAT ambayo vina lengo la kupunguza gharama za utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuongeza tija ya matumizi ya fedha za umma na kuhakikisha miradi inayotekelezwa kwa fedha za Serikali na za washirika wa maendeleo inakamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maji tayari imeshasambaza Waraka wa Hazina namba sita uliotolewa na Wizara ya Fedha na Mipango kuhusu utaratibu wa kutoa msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa miradi ya maji itakayotekelezwa kote nchini. Ni wajibu kwa Maafisa Masuuli wote kuzingatia utaratibu ulioainishwa na Serikali katika misamaha ya kodi kwa vifaa vya kusambazia maji ili miradi yetu ya maji ikamilike kwa wakati.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y MHE. LATHIFAH H. CHANDE) aliuliza:-

Serikali iliahidi Mji wa Liwale Kufanyiwa usanifu wa mradi wa maji:-

(a) Je, ni lini mradi huo uliofanyiwa usanifu utakamilika na kuanza kutoa huduma ya maji kwa wananchi wa Liwale?

(b) Je, ni kata zipi zilizopo katika Wilaya ya Liwale ambazo zitanufaika na mradi huo wa maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa ruksa yako kwanza naomba nitoe pole kwa wananchi wa Pangani na Chama cha Mapinduzi na wanaCCM wote kwa kuondokewa na Mzee wetu ndugu Hamis Mnegerwa ambaye ni Mwenyekiti wa chama chetu Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Pangani. Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi. Amin.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lathifah Chande, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya upatikanaji wa maji katika Mji wa Liwale ili kutatua changamoto hiyo, Serikali inatekeleza mipango ya muda mrefu na muda mfupi. Kwa upande wa muda mfupi katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imekamilisha mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji katika Mji wa Liwale.

Mheshimiwa Spika, kazi zilizotekelezwa katika mradi huo ni ukarabati wa kituo cha kusukuma maji, ununuzi na ufungaji wa pampu, ununuzi na ulazaji wa mabomba, usambazaji maji umbali wa kilometa 16 pamoja na ununuzi wa dira za maji 200 kwa gharama ya shilingi milioni 264. Kukamilika kwa mradi huo kumeongeza hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kutoka masaa matano kwa siku hadi masaa 12 kwa siku.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa muda mrefu, Serikali imepanga kufanya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa vitabu vya zabuni ambazo kazi hiyo imepangwa kufanyika mwaka wa fedha 2019/2020. Kukamilika kwa kazi hiyo kutatoa gharama halisi ya utekelezaji wa mradi mkubwa katika Mji wa Liwale pamoja na kuainisha kata zitakazonufaika na mradi huo.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-

Je, Serikali imetenga fedha kiasi gani ya ujenzi wa mabwawa ya maji ili kupunguza matatizo ya maji katika Wilaya ya Kilolo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Jimbo la Kilolo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Halmashauri ya Kilolo kw aupande wa Vijijini ni asilimia 71. Kilolo Mjini ni asilimia 80 na Ilula ni asilimia 47.5. Aidha, halmashauri ya Wilaya ya Kilolo imekamilisha ujen zi wa miradi ya vijiji 10 kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji pamoja na Ujenzi wa vijiji vitano kupitia ufadhili wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya WARIDI.

Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019, Halm ashauri ya Wilaya ya kilolo inatekeleza miradi ya maji katika vijiji vitatu vya Lundamatwe, Kitelewasi na Ilambo. Pia miradi miwili katika miji midogo ya Kilolo na Ilula. Aidha, Halmashauri ya Kilolo kwa kutumia fedha za ndani inakarabati mabwawa matatu yaliyopo katika vijiji vya Uhambingeto, Image na Mgowelo kwa ajili ya binadamu na mifugo.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na channgamoto ya uhaba wa maji kwa mwaka huu wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Kilolo imepokea jumla ya shilingi bilioni 1.7 ili kuhakikisha miradi ya maji inatekelezwa na kukamilika na kuwapunguzia keri ya maji wananchi wa wilaya hiyo.
MHE. DEO K. SANGA Aliuliza:-

Serikali ilikopa fedha za mkopo nafuu kutoka Serikali ya India kwa ajili ya miradi 26 ya maji ikiwemo Mji wa Makambako.

Je, ni lini mradi huo wa maji utaanza na kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepata mkopo wenye masharti nafuu wa dola za Marekani milioni 500 kutoka Serikali ya India kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji katika miji 28 kwa upande wa Tanzania Bara na mradi mmoja upande wa Zanzibar. Utekelezaji wa miradi hiyo umegawanyika katika awamu mbili; awamu ya kwanza ni usanifu na awamu ya pili ni ujenzi wa miradi husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Wizara imefikia katika hatua za mwisho za kumpata mtaalam mshauri kwa ajili ya kuandaa ripoti (detailed project report). Baada ya ripoti ya mradi kukamilika, Wizara itaendelea na hatua ya kutafuta wakandarasi kwa ajili ya ujenzi wa miradi. Ujenzi wa miradi hiyo unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2019/ 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wa kukamilika miradi hiyo utajulikana mara baada ya usanifu kukamilika.
MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:-

Benki ya Dunia imefadhili miradi ya visima kumi (10) katika kila wilaya nchini:-

Je, Serikali imefanya tathmini kujua asilimia ya miradi iliyofanikiwa na ambayo haikufanikiwa; na kwa ile ambayo haikufanikiwa, Serikali haioni haja ya kuingiza fedha ili kukamilisha miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016, Wizara ya Maji ilifanya tathmini ya kina nchi nzima ili kujua idadi ya visima vyote vilivyochimbwa kwa Awamu ya Kwanza ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji katika Halmashauri zote Tanzania Bara. Idadi ya visima vilivyochimbwa ni 1,485. Kati ya hivyo, visima 990, sawa na asilimia 67 vilipata maji na visima 495 sawa na asilimia 33 vilikosa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambayo visima vyake vilikosa maji Serikali ilitumia vyanzo vingine mbadala kama vile chemchemi, mito, maziwa au kujenga mabwawa ili kuhakikisha maeneo yaliyopewa kipaumbele katika mpango wa vijiji 10 yanapata huduma bora ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali imeanzisha Mfuko wa Maji wa Taifa ambao unalipa miradi yote iliyochelewa kukamilika na miradi mipya inayoendelea kujengwa katika Halmashauri zetu. Lengo ni kuhakikisha huduma bora ya maji kwa kila mwananchi.
MHE. CONCHESTER RWAMLAZA (K.n.y MHE. JOSEPH L. HAULE) aliuliza:-

Aliyekuwa Waziri wa Maji, Mheshimiwa Eng, Isack Kamwelwe, alitembelea chanzo cha maji cha Sigaleti kilichopo Kata ya Ruaha ambacho kimepimwa na kuthibitishwa na Wataalam wa Idara ya Maji kwamba, kina maji mengi na salama na kinaweza kuhudumia ipasavyo Kata za Ruaha, Kidodi na Ruhembe. Na kwamba, zinatakiwa shilingi bilioni 2 ili maji hayo yaweze kupatikana kwenye kata hizo:-

Je, Serikali ipo tayari kutenga kiasi cha fedha kwenye bajeti, ili kuokoa maisha ya wananchi zaidi ya 35,000?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mbunge wa Jimbo la Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kata za Ruaha, Kododi na Ruhembe ni miongoni mwa kata 18 zilizopo katika Jimbo la Mikumi. Upatikanaji wa huduma ya maji katika Jimbo hilo umefikia asilimia 68.

Mheshimiwa Spika, Kata za Ruaha, Kidodi n Ruhembe zina jumla ya vijiji 12, hata hivyo vijiji vinane tayari vimejengewa miundombinu ya miradi ya bomba; aidha vijiji vinne katika Kata ya Ruhembe vinatumia visima vifupi vilivyofungwa pampu za mkono, hivyo uboershaji wa huduma ya maji katika kata hizo bado ni muhimu kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wakazi na kukua kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, ni kweli chanzo cha maji cha Mto Sigaleti ni miongoni mwa vyanzo vya maji vinavyopendekezwa kutumika kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji katika Jimbo la Mikumi, zikiwemo kata hizo. Baada ya kupata makisio ya awali ya kiasi cha shilingi bilioni 2 kwa ajili ya kutekeleza mradi huo, kwa sasa Wizara yangu inafanya mapitio ya kina ya usanifu na alama na tayari kiasi cha shilingi milioni 658 kimetengwa katika mwaka wa fedha 2019/2020 kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huo.
MHE. ESTHER A. BULAYA aliuliza:-

Jimbo la Bunda Mjini limekuwa likikumbwa na adha ya ukosefu wa maji safi na salama na Serikali imekuwa ikikwamisha mradi wa maji safi na salama Bunda kwa muda sasa kushindwa kutoa fedha za utekelezaji:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha, ili mkandarasi aweze kukamilisha mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Amosa Bulaya, Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa Mji wa Bunda ni miongoni mwa maeneo ambayo yana shida kubwa ya maji. mahitaji ya maji kwa Wananchi wa Bunda mjini ni mita za ujazo 9,857 kwa siku wakati uzalishaji wa maji kwa sasa ni mita za ujazo 4,464 kwa siku. Hii inatokana na kutokukamilika kwa ujenzi wa miundombinu wa usambazaji maji baada ya mkandarasi kuondoka eneo la utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha mradi huo unakamilika na wananchi kuanza kunufaika na huduma ya maji, Serikali imechukua hatua kuainisha kazi zote ambazo hazijatekelezwa katika mradi huo, zinazogharimu kiasi cha shilingi milioni 375. Fedha hizo zinapelekwa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Musoma, ili ziweze kusimamia utekelezaji wa mradi huo na kuukamilisha, hivyo kuanza kuhudumia Wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini. Ni dhahiri kukamilika kwa mradi huu pamoja na ujenzi wa chujio jipya la maji kutasaidia kwa kiasi kikubwa kutatua tatizo la maji katika mji wa Bunda.
MHE. JOSEPH R. SELASINI aliuliza:-

Jimbo la Rombo hususan ukanda wa chini wenye takribani vijiji 41 lina shida ya maji; na Halmashauri imeanzisha mradi wa kupanua bomba kubwa la maji linalotoka Marangu. Aidha, Halmashauri ilipendekeza vyanzo vingine ikiwemo matumizi ya maji na Ziwa Chala, uchimbaji wa visima na mabwawa yatokanayo na mito ya msimu.

(a) Je, Serikali imekubali mpango wa kuanza kutumia maji ya Ziwa Chala?

(b) Je, ni lini Serikali itatoa fedha za kutosha ili mradi huo uweze kuanza?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Roman Selasini, Mbunge wa Jimbo la Rombo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali tayari ina mpango wa kutumia Ziwa Chala kama chanzo cha maji kwa wananchi wa Rombo. Uamuzi huo ulitokana na upembuzi yakinifu na usanifu uliofanyika kuanzia mwezi Machi, 2019 na kukamilika mwezi Julai, 2019. Upembuzi huo ulibainisha vyanzo vinne vya maji ambavyo ni chanzo cha maji cha Ziwa Chala kitakachohudumia vijiji 21 na vyanzo vingine vitatu vya maji vya mtiririko Mto Njoro, Mto Yona na Marangu na Uswai Wambushi.

Mheshimiwa Spika, makisio ya awali ya mradi huo ni shilingi bilioni 40 ambapo ujenzi wake uliamuliwa ufanyike kwa awamu. Awamu ya kwanza itahusu ujenzi wa chanzo cha maji cha Njoro ambacho kitahudumia Mji wa Tarakea na vijiji jirani na katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa mradi huo Serikali itaendelea kutenga fedha kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021 kwa ajili ya kukamilisha awamu ya kwanza na kuanza awamu nyingine.

Mheshimiwa Spika, baada ya awamu zote kukamilika mradi huu unatarajia kuhudumia vijiji vya Kikelelwa, Mbomai, Kibaoni, Nayeme, Nasae, Msanjai, Urauri, Ushiri, Ikuini, Mrao, Kiruakeni, Kisale, Marangu, Mamsera, Mahida, Holili, Mengwe na Ngoyoni vyenye jumla ya watu 157,000.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:-

Je, ni lini mradi wa maji kwa ajili ya Kyaka – Bunazi utaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Dkt. Diodoras Buberwa Kamala, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika katika juhudi za kuboresha huduma ya maji katika Kata za Kyaka na Bunazi, Serikali ilibuni mradi wa maji ambao utawahudumia wananchi wa kata hizo. Usanifu wa mradi na taratibu za ununuzi wa Mkandarasi wa ujenzi wa mradi huo zimekamilika. Utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Kyaka-Bunazi umepangwa kutekelezwa katika mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kuu zilizopangwa kutekelezwa kwenye mradi huo ni ujenzi wa tekeo la maji litakalojengwa katika mto Kagera eneo la Rubale, ulazaji wa bomba kuu urefu wa kilomita 1.5, mtambo wa kutibu maji na Tanki la kuhifadhia maji lenye lita milioni mbili litakalojengwa katika eneo la Kituntu. Mradi huu ukimalika unatarajiwa kuhudumia jumla ya wakazi wote wa kata za Kyaka na Bunzai wapatao 64,470.
MHE. RICHARD M. NDASSA (K.n.y. MHE. KISWAGA B. DESTERY) aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia mtandao wa maji Magu kupeleka Tarafa ya Ndagalu, Kata za Shishani, Njinjinili, Kabila, Nkungulu, Ng’haya, Sukuma, Buhumbi na Mwamabanza zenye jumla ya vijiji 24?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Magu Mjini ambao tayari umekamilika, una uwezo wa kuzalisha maji kiasi cha lita milioni 7.25 kwa siku, ukilinganisha na mahitaji ya sasa ya lita milioni 3.54 kwa wakazi wa Magu Mjini na Vijiji vya Kipeja, Sagani, Nyashimba na Ilungu. Hivyo Mradi huu una ziada ya maji ya lita milioni 3.71 kwa siku kwa sasa kutokana na ziada hiyo, Serikali kupitia Programu ya lipa kwa matokeo yaani Programme for Results (P4R) itajenga miundombinu ya usambazaji wa maji kutoka kwenye Mradi wa Magu mjini kupeleka kwa baadhi ya vijiji vilivyopo tarafa ya Ndagalu ikiwa ni pamoja na Vijiji vya Misungwi, Kitongo, Lumeji, Buhimbi, Iseni, Nyang’hanga na Nyashoshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kuwa azma ya upatikanaji wa maji katika vijiji vingine vya Tarafa ya Ndagalu inapatiwa ufumbuzi wa kudumu, Serikali itahakikisha kuwa imetenga fedha katika bajeti ya Mwaka 2020/2021 ili vijiji vilivyobaki viweze kupata huduma ya maji kupitia Mradi wa Ziwa Victoria.
MHE. ALMAS A. MAIGE aliuliza:-

Serikali inatekeleza mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria na kuyapeleka Mkoa wa Tabora katika Miji ya Igunga, Nzega, Manispaa ya Tabora, Sikonge, Isikizya na Urambo:-

(a) Je, ni vijiji gani vya Mashariki vya Jimbo la Tabora Kaskazini – Uyui vitapatiwa maji kutokana na mradi huo?

(b) Kwa vile ni idadi ndogo tu ya vijiji kati ya 82 vya Jimbo la Tabora Kaskazini ndiyo vitapatiwa maji na mradi huo: Je, Serikali ina mpango gani wa kuvipata maji vijiji vyote katika Jimbo la Tabora Kaskazini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatekeleza mradi wa kutoa maji Ziwa Victoria kwenye Miji ya Tabora, Igunga na Nzega pamoja na vijiji zaidi ya 102 vilivyopo umbali wa kilomita 12 kila upande kutoka bomba kuu. Vijiji vilivyopo Jimbo la Tabora Kaskazini katika mradi huu ni 26 ambavyo ni Igoko, Isikizya, Ikonolo, Mswa, Itobola, Isenegenzya, Majengo, Ikongolo, Kanyenye, Kiwembe na Kalemela,

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali imeanza kutekeleza miradi katika miji 28 kupitia mkopo wa Dola za Marekani milioni 500 kutoka Benki ya Exim ya India. Mradi huo utapeleka maji katika Miji ya Sikonge, Urambo, Kaliua na baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Uyui kwa kutoa maji Ziwa Victoria. Mpaka sasa vijiji vilivyotambuliwa wakati wa usanifu wa kupeleka maji Sikonge, Urambo na Kaliua ni 14 ambavyo ni Kasisi B, Ilalongulu, Mpenge, Isenga, Ngokolo, Ulimakafu, Mabama, Tumaini, Maswanya, Chali Ndono, Itinka, Tulieni na Utemini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, kwa miradi yote miwili itahudumia jumla ya vijiji 40 vya Jimbo la Tabora Kaskazini. Serikali itaendelea kutenga na kutoa fedha ili kuhakikisha vijiji vyote vilivyobaki vinapata huduma ya maji.
MHE. SUSANNE P. MASELLE aliuliza:-

Bado kuna shida kubwa ya upatikanaji wa maji kwa wananchi wetu hasa maeneo ya vijijini:-

Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu kupunguza au kumaliza tatizo hilo kwa wananchi wa maeneo mbalimbali ya Misungwi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susanne Peter Maselle, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto ya maji kwa wananchi wa maeneo mbalimbali ya Misungwi, Serikali imekamilisha ujenzi wa mradi wa maji wa thamani ya shilingi bilioni 12.85 kutoka katika chanzo cha maji cha Nyahiti ambapo wakazi wapato 64,280 wanatarajia kunufaika katika mradi huo hadi kufikia mwaka 2040.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mradi huo, Serikali inatekeleza mradi mkubwa kutoka bomba kuu la usafirishaji maji la KASHWASA utakaohudumia vijiji 14 vya Wilaya ya Misungwi kupitia miradi mitano. Mradi wa kwanza ni kufikisha huduma ya maji Mabale – Mbarika, mradi wa pili ni kufikisha huduma ya maji Igenge, mradi wa tatu ni kufikisha huduma ya maji Mbarika – Ngaya, Mradi wa nne ni kufikisha huduma ya maji Ngaya – Matale na mradi wa tano ni kufikisha huduma ya maji Matale – Misasi. Miradi hii ikikamilka itahudumia jumla ya watu 45,788.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali imeanza kutekeleza miradi katika vijiji vitano vya Kata ya Shilalo kupitia Programu ya Malipo kwa Matokeo, inayofadhiliwa na Benki ya Dunia. Miradi hiyo ikikamilika itahudumia watu wapatao 15,500. (Makofi)
MHE. FELISTER A. BURA aliuliza:-

Kutokana na Serikali kuhamia Dodoma, mahitaji ya maji safi na salama yamekuwa makubwa na kwa sasa mgao wa maji kwa wakazi wa Dodoma umeshaanza:-

Je, Serikali ina mpango gani mahsusi wa kuhakikisha wakazi wa Dodoma wanapata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, chanzo kikubwa cha uzalishaji maji kwa matumizi ya wakazi wa Jiji la Dodoma ni visima virefu vilivyochimbwa katika Bonde la Makutopora eneo la Mzakwe. Kuna jumla ya visima vya uzalishaji maji 24 na visima vitano vya kuchunguza mwenendo wa maji ardhini (observation boreholes) vimechimbwa katika bonde hilo. Uwezo wa visima vilivyopo Mzakwe kwa sasa pamoja na uwezo wa usafirishaji wa maji ni mita za ujazo 61,500 kwa siku.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha huduma ya maji inakuwa ya uhakika, Serikali kupitia Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Jijini Dodoma, imeongeza chanzo kingine cha maji eneo la Ihumwa chenye uwezo wa kuzalisha maji mita za ujazo 2,773 kwa siku. Chanzo hiki kina visima nane na kinahudumia Mji wa Serikali uliopo Mtumba pamoja na Kijiji cha Ihumwa.

Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuboresha huduma ya maji, kwa mpango wa muda mfupi Serikali inaendelea na utafiti wa maji chini ya ardhi na uchimbaji wa visima virefu katika Mitaa ya Ntyuka, Michese na Nala na uendeshaji wa visima nane katika Mji wa Chamwino. Mpango wa muda wa kati wa ujenzi wa Bwawa la Maji la Farkwa litakalotumika kama chanzo cha nyongeza cha majisafi katika Jiji la Dodoma.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-

Halmashauri ya Mbeya ina upungufu mkubwa wa maji karibu kwenye Vijiji zaidi ya 153 na hasa katika Kata ya Mjele. Je, Serikali ina mpango gani wakupeleka maji kwenye Vijiji hivyo na hasa Vijiji vya Mjele, Chang‟ombe na Ipwizi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njenza, Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua tatizo la maji lililopo katika Halmashauri ya Mbeya Vijijini, katika mwaka wa fedha wa 2019/2020, Serikali imepanga kutekeleza miradi tisa ya maji ambayo ni Idimi - Haporoto, Iwindi, Mshewe, Ipwizi, Mjele - Chang‟ombe, Galijembe, Nsenga - Wimba, Iyawaya na Isangala group . Kiasi cha shilingi bilioni 6.4 kimetengwa katika bajeti ya 2019/20 kwa ajili ya kazi hiyo. Hadi kufikia mwezi Disemba 2019, jumla ya miradi 2 ya Idimi - Haporoto na Iwindi imekamilika na kiasi cha fedha shilingi bilioni 1.5 kimetumika katika ujenzi wa miundombinu ya maji.

Mheshimiwa Spika, baada ya Serikali kukamilisha miradi yote iliyopo kwenye bajeti ya 2019/2020, jumla ya vijiji 21 vitapata huduma ya maji vikiwemo vijiji vya Mjele, Chang‟ombe na Ipwizi ambapo jumla ya wakazi wapatao 44,364 watanufaika.
MHE. BUPE N. MWAKANG‟ATA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga visima virefu vya maji katika Wilaya ya Nkasi ili kutatua changamoto ya maji iliyopo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang‟ata Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua tatizo la maji lililopo katika Wilaya ya Nkasi Serikali katika mwaka wa fedha 2019/2020 imepanga kuchimba visima virefu 9 katika maeneo ya Masolo, Katogolo, Mpata, Mienge, Itindi, Kacheche, Lyele, Mbwendi na Kakoma. Kiasi cha shilingi milioni 315 kimetengwa katika bajeti ya mwaka 2019/2020 kwa ajili ya kazi hiyo. Hadi kufikia mwezi Disemba 2019, Visima 7 vimechimbwa katika vijiji vya Masolo, Katogolo, Mpata, Mienge, Kanazi na Ipanda na kiasi cha shilingi milioni 220 kimetumika katika upimaji na uchimbaji wa visima hivyo ambavyo vitatumika kama vyanzo vya maji katika vijiji husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa muda mrefu wa kutatua tatizo la maji katika Wilaya ya Nkasi, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imepanga kutumia zaidi ya bilioni 1.3 kwa kupitia Programu ya PforR kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji katika Wilaya ya Nkasi. Wizara imeshatuma fedha hizo kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji 6 Wilayani Nkasi ambapo miradi yote hiyo itatekelezwa kwa mfumo wa wataalam wa ndani (Force Account).
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-

Jimbo la Tunduru Kusini lina changamoto ya maji kutokana na mabadiliko ya tabianchi:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuchimba visima virefu na vifupi katika kata ya Tuwemacho, Mchuluka, Mchoteka, Mbati, Marumba, Wenje, Nasomba, Namasakata na Lukumbule.
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa maji naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate Mbunge wa Tunduru Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa Jimbo la Tunduru Kusini lina jumla ya miradi mitano ya maji ya bomba kwenye vijiji 11. Miradi hiyo ipo kwenye Kata za Mbati, Nalasi, Namasakata, Misechela, Mtina, Ligoma, Mchesi na Lukumbule. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika Sekta ya Maji Help for Underserved Communities imechimba visima 72 katika Kata za Tuwemacho, Marumba, Lukumbule Mbesa na Mtina. Visima hivyo vimefungwa pampu za mkono. Vilevile Wilaya ya Tunduru kwa kushirikiana na wadau wa Maendeleo ya Sekta ya Maji All Mother and Child Count imechimba visima virefu katika kata za Mchuluka, Namasakata, Chiwana na Lukumbule. Visima hivyo vitatumika kujenga miradi ya maji ya bomba katika maeneo hayo. Tayari utekelezaji umeanza kwa kata ya Chiwana na Namasakata

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha huduma ya maji inakuwa ya uhakika katika Wilaya ya Tunduru, Serikali kupitia Wakala ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini imetenga na kutoa fedha katika bajeti ya mwaka 2019/2020 kiasi cha shilingi milioni 974 kwa ajili ya kujenga, kukarabati na kufanya upanuzi wa miradi ya maji katika vijiji mbalimbali vilivyopo wilaya hiyo vikiwemo vijiji vya Jimbo la Tundurru Kusini. Vijiji hivyo ni Mbesa, Airport, Nasomba, Namasakata, Chiwana, Semeni, Nalasi, Misechela, Angalia, Ligoma na Mchekeni. Aidha, Serikali imepanga kuchimba visima Virefu viwili katika vijiji vya Wenje na Likweso vilivyopo Jimbo la Tunduru Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga na kutoa fedha kadri zinavyopatikana ili kuweza kujenga na kukarabati miradi ya maji katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Jimbo la Tunduru Kusini ili wananchi waweze kunufaika na huduma ya majisafi na usafi wa mazingira.
MHE. AYSHAROSE N. MATEMBE aliuliza:-

Mradi wa maji wa Kitinku/Lusilile ndiyo uliotarajiwa kuwa mkombozi wa Wananchi wa Manyoni katika kupata huduma ya maji safi na salama, lakini mradi huo kwa muda mrefu umekwama kutokana na fedha kutopelekwa:-

Je, Serikali ina mikakati gani ya kukamilisha mradi huo muhimu kwa wakati ili kumtua ndoo kichwani Mwanamke wa Manyoni?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Matembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Kintinku Lusilile ulibuniwa kwa lengo la kuhudumia vijiji 11 vyenye wakazi wapatao 55,485 kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012. Vijiji hivyo ni Kintinku, Lusilile, Maweni, Mvumi, Ngaiti, Chikuyu, Mwiboo, Mbwasa, Mtiwe, Makutupora na Chilejoho. Kwa mujibu wa usanifu uliofanyika mradi huu unakadiriwa kugharimu bilioni 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa mradi huu umepangwa skutekelezwa katika awamu nne ambapo awamu ya kwanza ilihusisha utafiti na uchimbaji wa visima vinne na utekelezaji wake ulikamilika. Hivi sasa utekelezaji wa awamu ya pili unaendelea ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni tarehe 23 Mei, 2018 iliingia mkataba na Mkandarasi CMG Construction Company Limited kutekeleza awamu ya pili ya mradi huo ambao ulitarajiwa kukamilika mwezi Novemba, 2018. Hata hivyo kutokana na changamoto ya upatikanaji wa fedha awamu hiyo haukuweza kukamilika kama ilivyopangwa na kwa sasa utekelezaji wa awamu ya pili umepangwa kukamilika mwezi Septemba 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mikakati ya kuhakikisha tunaongeza kiwango cha upatikanaji wa maji katika Wilaya ya Manyoni, Wizara imetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.4 kwenye mwaka wa fedha 2019/2020 kutekeleza miradi mbalimbali ya maji wilayani humo. Tayari RUWASA wamewasilisha maombi ya kuanza kutekeleza awamu ya tatu ya Mradi wa Maji wa Kintinku/Lusilile.
MHE. DAVID E. SILINDE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani kwa sasa kutatua kero ya maji kwa uhakikia katika Jimbo la Momba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika juhudi za kutatua tatizo la maji katika Jimbo la Momba, Serikali inaendelea kutekekeza miradi mitatu katika Vijiji vya Ndalambo ambapo ujenzi umekamilika kwa asilimia 95, Kijiji cha Chitete ujenzi umekamilika kwa asilimia 12 na Tindingomba ujenzi umekamilika kwa asilimia 80. Miradi hii ikikamilika, itahudumia jumla ya watu wapatao 23,397 na kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi, salama kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali imeanza kutekeleza miradi ya vijiji vitano kupitia Programu ya Malipo kwa Matokeo (PfR) katika Vijiji vya Mkulwe, Chiwanda, Kasinde, Ikana na Namsinde II kwa gharama ya Sh.805,885,340. Kukamilika kwa miradi hii, kutawezesha jumla ya watu 31,984 kupata huduma ya maji.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA aliuliza:-

Mradi wa maji katika Kata ya Mtwango bado haujakamilika:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi huo ambao umechukua muda mrefu bila kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako kwanza naomba nitoe pole kwa wananchi wa Jimbo langu la Pangani pamoja na wananchi wa Mkoa wa Tanga kwa mafuriko ambayo yalikuwa yametokea, tumepoteza ndugu zetu lakini pia kuharibika kwa miundombinu. Tunamshukuru Mkuu wa Mkoa kwa hatua ya haraka ya kuweza kurejesha miundombinu ile.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mendrad Lutengano Kigola, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mradi wa Maji wa Kata ya Mtwango umechukua muda mrefu kutokana na changamoto iliyokuwepo ya wakandarasi kutokamilisha kazi kwa wakati hali ambayo ililazimu kuwaondoa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, Serikali imetenga shilingi milioni 300 kwa lengo la kukamilisha mradi huo. Kazi zitakazofanyika ni ujenzi wa matenki, ununuzi wa pampu na ununuzi wa mabomba ya kusambaza maji kwa wananchi. Kazi hizo zitafanywa na wataalam na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini yaani RUWASA katika ngazi ya wilaya na mkoa. Taratibu za kukamilisha kazi zilizobaki katika Kijiji cha Sawala zinaendelea. Mradi huo unategemewa kukamilika katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. JAMES K. MILLYA aliuliza:-

Kuna mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka Mkoa wa Kilimanjaro kuelekea Arusha Mjini, mradi huu unapitia kwenye mipaka ya Wilaya ya Simanjiro Kata za Naisinyai na Mererani.

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Wananchi wa Kata hizo wanapatiwa huduma hiyo inayopita kwenye maeneo yao;

(b) Mheshimiwa Rais alipokuwa akizindua ujenzi wa barabara ya kilometa 14 toka KIA hadi Mererani aliwaahidi Wananchi wa Mererani na Naisinyai kwamba atawakumbuka kwenye kuondoa adha ya maji; Je, Serikali imejipangaje kutimiza ahadi hiyo ya Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa James Kinyasi Millya Mbunge wa Simanjiro lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mradi wa kuboresha huduma ya maji katika Jiji la Arusha na baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Arumeru. Mradi huu pia utatoa huduma ya maji katika maeneo ambayo bomba kuu la maji kuelekea Arusha litapita. Kata za Mererani na Naisinyai ni miongoni mwa kata hizo na vijiji vitakavyopata huduma ya maji ni Naepo, Oloshonyoke na Kibaoni ambavyo viko katika Kata ya Naisinyai na vijiji vya Songambele, Getini na Kangaroo ambavyo viko katika Kata ya Mererani.

Mheshimiwa Spika, katika kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kuondoa adha ya maji katika maeneo hayo, mradi wa kuboresha huduma ya maji katika Jiji la Arusha na baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Arumeru utahusisha kuboresha huduma ya maji katika kata za Mererani na Naisinyai. Mradi huu mkubwa wa maji kutoka Kilimanjaro kwenda Jiji la Arusha unatarajia kukamilika mwezi Juni, 2020. Mradi utakapokamilika, adha ya maji katika maeneo hayo itakuwa ni historia.
MHE. DKT. MARY M. NAGU aliuliza:-

Je, ni lini miradi ya visima vya Waranga, Dumbeta, Endamudagya, Gidika, Murumba na Hirbadaw itakamilika na kuanza kusambaza maji kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mary Michael Nagu Mbunge wa Hanang kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutatua changamoto ya maji katika vijiji vya Waranga, Dumbeta, Endamudagya, Gidika, Murumba na Hirbadaw, Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018 ilichimba visima vitano (5) vyenye uwezo wa kuzalisha maji kiasi cha mita za ujazo 45 kwa saa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha visima hivyo vinatoa huduma ya maji kwa wananchi, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali kupitia Programu ya Usambazaji Maji Endelevu Vijjini na Usafi wa Mazingira imetenga Kiasi cha Shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya usambazaji maji katika vijiji vya Dumbeta, Waraga na Hirbadaw. Aidha, jumla ya vituo 30 vya kuchotea maji vitajengwa katika vijiji hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji katika visima vingine vilivyobakia vya Gidika, Endamudagya na Murumba utafanyika katika mwaka ujao wa fedha 2020/2021.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA aliuliza:-

Mradi wa Maji unaotekelezwa chini ya Programu ya WSDP katika Vijiji vya Malinyi, Kipingo na Makerere unasuasua sana toka 2015 hadi sasa mradi huo haujakamilika:-

(a) Je, ni lini mradi huo utakamilishwa ili kuwawezesha wakazi wapatao 18,000 wa vijiji hivyo kupata maji safi na salama?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapelekea maji wakazi wa Vijiji vya Miembeni, Mchangani na Misegese Kata ya Malinyi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Hadji Hussein Mponda, Mbunge wa Jimbo la Malinyi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuanzia mwaka 2015, Serikali inatekeleza mradi wa maji wa Malinyi unaotarajia kuhudumia Vijiji vya Kipingo, Makerere na Malinyi ambapo ni Makao Makuu ya Wilaya. Ujenzi wa mradi huo unagharimu shilingi bilioni 3.01. Hadi kufikia mwezi Oktoba, 2019, utekelezaji wake umefikia asilimia 80. Kazi zilizofanyika ni ujenzi wa miundombinu ya chanzo cha maji, ulazaji wa bomba kuu la maji urefu wa kilomita 22, ujenzi wa tanki la lita 150,000, vituo vya kuchotea maji 47 na ulazaji wa mabomba ya usambazaji maji kwa umbali wa kilomita 14.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kukamilika kwa kazi hizo, miundombinu hiyo imeshindwa kufikisha huduma ya maji kwa wananchi kutokana na upungufu katika usanifu wa mradi. Serikali imemwagiza Mtaalam Mshauri anayesimamia ujenzi wa mradi huo kufanya marekebisho ili wananchi waweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Vijiji vya Mwembeni, Misegese na Mchangani kuna visima virefu viwili vyenye maji ya kutosha. Hivyo, kwa mwaka huu wa fedha 2019/2020 Serikali itafanya usanifu ili kuviendeleza visima hivyo ili kuboresha huduma ya maji kwa wananchi wa vijiji hivyo. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-

Je, ni kwa kiasi gani Serikali imeweka mikakati ya kuhamasisha uvunaji wa maji ya mvua ili kupunguza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi hasa ikizingatiwa kuwa Tanzania kijiografia ipo katika ukanda wenye mvua za kutosha?
NAIBU WAZIRI WA MAJI, alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo kimojawapo katika kuongeza uhakika wa upatikanaji wa maji kwa wananchi ni maji ya mvua. Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ilizielekeza Mamlaka za Serikali za Mtaa kutunga sheria ndogo ndogo ili kuhamasisha na kushauri kuwa nyumba zote zinazojengwa ziwekewe miundombinu kwa ajili ya uvunaji wa maji ya mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa uhaba wa maji bado ni changamoto katika nchi yetu, Serikali inaendelea kuhimiza na kuhamasisha jamii kwa kutoa elimu ya utaratibu wa uvunaji wa maji ya mvua kwa kutumia njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na ujenzi wa mabwawa, malambo na uvunaji wa maji ya paa. Katika utekelezaji wa Programu ya kuendeleza Sekta ya Maji nchini, uhamasishaji umefanyika kwa kujenga matenki ya mfano ya kuvuna maji ya mvua katika maeneo ya shule na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Maji imeandaa Mwongozo wa Uvunaji wa Maji ya Mvua ambao utasambazwa na kutumika nchi nzima. Mwongozo huo umeainisha mbinu mbalimbali za kuvuna maji ya mvua katika Kaya na Taasisi. Mwongozo utatumika katika kupanga, kusanifu, kujenga na uendeshaji na matengenezo ya miundombinu ya uvunaji wa maji ya mvua. (Makofi)
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:-

Ujenzi wa Bwawa la Matwiga Wilayani Chunya umechukua zaidi ya miaka mitano bila kukamilika:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Victor Mwambwalaswa, Mbunge wa Jimbo la Lupa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Chunya ni miongoni mwa wilaya zenye asilimia ndogo ya upatikanaji wa huduma ya maji vijijini. Changomoto hii inatokana na wilaya hiyo kuwa na uhaba mkubwa wa vyanzo vya maji ikiwemo mito na chemchem ambazo zingeweza kutumiwa kuhudumia wananchi. Aidha, wilaya hii pia inakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji chini ya ardhi. Kwa kutambua hilo, Serikali ilianza ujenzi wa mradi wa maji wa Bwawa la Matwiga kwa lengo la kusaidia kupunguza shida ya maji iliyopo. Utekelezaji wa mradi huo ulipangwa katika awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ilijikita katika ujenzi wa bwawa lenyewe kama chanzo cha maji na awamu ya pili ni ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji kutoka kwenye bwawa kwenda kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa awamu ya kwanza inayohusisha ujenzi wa bwawa lenyewe imekamilika ambapo bwawa hilo lina uwezo wa kuhifadhi maji lita 248,000,000 kwa mwaka. Hata hivyo, mnamo mwaka 2018 kulikuwepo na changamoto ya mvua kubwa iliyopekelea kuharibika kwa sehemu ya utoro wa maji (Spillway) ambayo kwa sasa mkandarasi (DDCA) yupo eneo la kazi na anaendelea na marekebisho ambapo kabla ya msimu wa mvua za mwaka huu kazi hiyo itakuwa imekamilika.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza utekelezaji wa awamu ya pili inayohusu ujenzi wa miundombinu ya kupeleka maji kwa wananchi. Ili kutumiza azma hiyo, Serikali imengia mkataba na Mtaalam Mshauri, BICO kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kufanya usanifu wa miundombinu ya kusambaza maji. Hadi sasa Mtaalam Mshauri huyo amewasilisha taarifa ya awali ya usanifu wa miundombinu ya kusambaza maji katika vijiji vinne (4) vya Kata za Matwiga na Mtanila. Kukamilika kwa hatua ya usanifu kutawezesha Serikali kutenga na kupeleka fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji.
MHE. MARIA N. KANGOYE Aliuliza:-

Kumekuwa na mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kuelekea Mikoa ya Shinyanga na Tabora vyenye mitambo yake chanzo cha maji kule Ihelele Wilayani Misungwi, aidha maeneo yanayozunguka mitambo hiyo na yanayopitiwa na mabomba ya mradi huo hayana maji safi na salama.

Je, nini mpango wa Serikali kusambaza maji safi na salama kutoka Ziwa Victoria kwa wananchi wa vijiji vya Mkoa wa Mwanza hususan maeneo yanayopitiwa na bomba hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndila Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa maji kutoka Ziwa wa Victoria, Serikali ililenga kufikisha maji katika miji ya Kahama na Shinyanga na vijiji vyote vilivyopo kando ya bomba kuu la kusafisha maji. Kwa wakati huo vijiji vilivyokidhi na kuingizwa katika mradi huu vilikuwa ni vijiji vilivyopo umbali usiozidi kilometa tano kwa kila upande wa bomba kuu. Hivyo, jumla ya vijiji 39 vikiwemo vijiji vitano vya Mawile, Ilalambogo, Lubili, Isenengeja na Ibinza vya Wilaya ya Misungwi katika Mkoa wa Mwanza viliunganishwa na vilianza kupata huduma a maji tangu uendeshaji wa mradi ulipoanza mwezi Februari, 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo cha maji na mitambo ya kusafisha maji kwa mradi wa Kahama - Shinyanga iko katika kijiji cha Nyang’ohomango. Aidha, eneo hilo pia linapakana na vijiji vya Lubili, Isesa, Igenge na Mbalika. Kwa kutambua umuhimu wa maeneo haya kuwa na huduma ya majisafi na salama kwa mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali ilianza ujenzi wamradi wa maji vijiji vya Nyang’ohomango, Isesa, Igenge na Mbalika kwa gharama ya shilingi bilioni 6.1.

Aidha, fedha za kutekeleza mradi huu zinatolewa kwa asilimia mia moja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Inatarajiwa kuwa baada ya ujenzi huo kukamilika, jumla ya wananchi 14,606 wa vijiji hivyo na mifugo yao watanufaika na huduma ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa mradi huu kutawezesha pia kuunganishwa kwa mradi wa maji unaoanzia kwenye kijiji cha Mbalika kwenda katika mji wa Misasi katika Wilaya ya Misungwi ambao pia utahudumia ziadi ya vijiji kumi.
MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD Aliuliza:- Serikali iliahidi kuleta mradi wa maji katika Jimbo la Morogoro Mjini ambao utamaliza kero ya maji katika maeneo mbalimbali ikiwemo Kihonda, Tungi, Lukombe na Mkundi katika Kata ya Mindu.

(a) Je, ni lini mradi huo utaanza?

(b) Je, mradi huo unategemewa kugharimu kiasi gani?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdul-Aziz Mohamed Abood, Mbunge wa Morogoro Mjini lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali iliahidi kutekeleza miradi mbalimbali kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji katika Jimbo la Morogoro Mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza ahadi hiyo, Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA) imeandaa mipango ya muda mfupi na mrefu. Katika mipango ya muda mfupi katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetekeleza mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji katika Kata za Kihonda na Mkundi. Mradi huo umegharimu kiasi cha shilinigi bilioni 1.9 na umewanufaisha wakazi wapatao 17,000 wanaoishi maeneo ya Kihonda, Kilimanjaro, Kiyegea na Kihonda Kaskazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Ufaransa kupita Shirika lake la Maendeleo la AFD itatekeleza mradi wa kuboresha huduma ya maji safi katika Manispaa ya Morogoro. Kazi zitakazotekelezwa ni kuongeza kina cha Bwawa la Mindu, ujenzi wa mtambo wenye uwezo wa kusafisha na kutibu maji, upanuzi wa matandao wa kusambazi maji, ukarabati wa mabwawa ya majitaka. Gharama ya mradi huo ni Euro milioni 70. Taratibu zakusaini mkataba wa kifedha zinaendelea na zitakapokamika utekelezaji wa mradi utaanza.
MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA Aliuliza:-

Serikali ilitoa zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji ya Nyabibuye, Gwanumpu, Muhange, Kiduduye, Nyangwijima na Kakonko Mjini. Miradi hiyo sasa inahitaji ukarabati mkubwa hata kabla ya kuanza uzalishaji na mingine utekelezaji upo chini ya asilimia 10:-

(a) Je, ni kasoro gani zimesababisha miradi yote sita kutotekelezwa kwa mwaka uliopangwa?

(b) Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha miradi hiyo inakamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Christopher Chiza Mbunge wa Buyungu, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa miradi ya Muhange, Kiduduye na Nyangwijima ulikamilika lakini ulishindwa kuwanufaisha wananchi kutokana na kasoro mbalimbali zilizojitokeza ikiwemo eneo la kisima cha pampu cha mradi wa Muhange kujaa tope; na pia kwa mradi wa maji Nyagwijima na Kiduduye eneo la chanzo kushindwa kuzuia maji kuyapeleka kwenye kisima chenye pampu hii imetokana na matatizo ya usanifu yaliyojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha miradi hii inatoa huduma kwa wananchi kama ilivyokusudiwa, Serikali imechukua hatua mbalimbali kwa miradi ya Muhange, Kiduduye na Nyagwijima, Wizara imefanya mapitio ya usanifu ambapo kiasi cha shilingi milioni 300 kimekadiriwa ili kurekebisha kasoro zilizojitokeza. Tayari Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 120 kwa ajili ya maboresho ya mradi wa maji Muhange ambapo utekelezaji unaendelea na umefikia asilimia 45. Serikali itaendelea kutenga na kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha pia miradi ya Nyagwijima na Kiduduye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya maji Gwanumpu, Nyabibuye na Kakonko Mjini utekelezaji wake ulichelewa kutokana na wakandarasi kujenga miradi hiyo kwa kasi ndogo kutokana na uwezo mdogo wa kifedha. Hali hii ilisababisha baadhi kusitishwa mikataba yao. Mkandarasi wa Mradi wa Gwanumpu yupo eneo la mradi na anaendelea na kazi ambapo amefikia asilimia 40. Kwa Mradi wa Maji wa Nyabibuye na Kakonko Mjini taratibu za kusaini mikataba na wakandarasi wapya zinaendelea ili waweze kukamilisha utekelezaji wa miradi hiyo.
INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:-

Usanifu na upembuzi wa kina wa mradi wa maji wa vijiji 57 Wilayani Kyerwa umekamilika muda mrefu. Je, ni lini utekelezaji wa mradi huo utaanza ili wananchi wa Kyerwa waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba nitoe pole kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga kwa kuondokewa na kipenzi chetu aliyekuwa Mbunge Mheshimiwa Omary Nundu Mwenyezi Mungu ailaze mahala pema roho yake peponi.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Jimbo la Kyerwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wialya ya Kyerwa ni mojawapo ya wilaya zinazounda Mkoa wa Kagera na kwa sasa hali ya upatikanaji wa huduma ya maji imefika asilimia 45.6 kutokana na asilimia ya upatikanaji wa huduma ya majisafi na salama kuwa Serikali iliamua kubuni mradi mkubwa utakaoweza kuhudumia wananchi zaidi ya 232,000 walioko kwenye vijiji 57 kutoka kwenye chanzo kimoja ambacho ni Ziwa Rushwa kando na Mto Kagera. Kazi hii alipewa mtaalam mshauri Don Consult na aliweza kukamilisha kazi hiyo mwaka 2018.

Mheshimiwa Spika, taarifa ya usanifu pamoja na makisio ua utekelezaji wa mradi huo ni shilingi bilioni 144.

Baada ya kupitia gharama hizo, Serikali imeamua kupitia upya usanifu huo ili kujiridhisha na mfumo wa ujenzi uliopendekezwa na gharama za ujenzi wa mradi huo. Serikali imeamua kuchukua hatua na uamuzi huo kutokana na uzoefu ulipatikana kuwa baadhi ya miradi mikubwa imekuwa na gharama kubwa bila kuzingatia uhalisia wa teknolojia inayopendekezwa na pia uwezo wa uendeshaji wa jamii husika.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo wakati taratibu hizo zinaendelea, Serikali kwa upande wake inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo kwa kadri mapitio ya usanifu yatakavyoonesha na utatekelezwa kwa awamu. Kwa kuanza, mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga shilingi bilioni moja zitakazoanza kutekeleza mradi huo kwa awamu kwenye vijiji vya Mkiyonza, Nshunga, Milambi, Mkombozi, Rukuraijo, Nyabikurungo na Nyaruzumbura. Hivyo, Serikali inamuomba Mheshimiwa Mbunge kuwa mvumilivu wakati Serikali inaendelea kukamilisha mapitio ya usanifu kwa lengo la kuanza kutekeleza mradi huo.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-

Mwaka 2018 ulikuwa msimu wa mvua nyingi sana zilizosababisha kubomoka kwa mabwawa ya maji kwenye Kata za Kinungu, Nguvumoja, Mwamashimba, Nanga, Bukoko na Mbutu na kuwaacha wananchi wa vijiji zaidi ya 24 bila maji; maeneo haya ni mbuga na hayana maji chini ya ardhi hivyo wananchi hutegemea mabwawa hayo tu. Aidha, Halmashauri ya Igunga haina uwezo wa kifedha kuyakarabati mabwawa hayo mara moja:-

Je, ni kwa nini Serikali isilete mradi mkubwa wa kukarabati miundombinu ya maji katika kata hizo kuwaondolea wananchi hao tabu ya maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Jimbo la Igunga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mwaka 2018 kulikuwa na mvua nyingi zilizonyesha na kuharibu miundombinu ya malambo katika Kata za Kinungu, Nguvumoja, Mwamashimba, Nanga, Bukoko na Mbutu na kuwaacha wananchi wa vijiji zaidi ya 24 bila ya huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, Serikali tayari inaendelea na ujenzi wa mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka bomba kuu la KASHWASA kupeleka katika Miji ya Tabora, Igunga, Nzega na Wilaya ya Uyui, ambao unatekelezwa kwa gharama za dola za Marekani milioni 268.35, fedha ambazo mkopo wa masharti nafuu kutoka Serikali ya India. Katika mradi huo vipo vijiji mbalimbali vya Kata Nanga na Mbutu zitapata huduma ya maji kupitia mradi huo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kukarabati miundombinu iliyoharibiwa na mvua hizi kwa Kata za Kinungu, Nguvumoja, Mwambashimba na Bukoko kwa kadri fedha zinavyopatikana ili kuhakikisha wananchi hawa wanapata huduma ya maji kama ilivyokuwa awali.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza:-

Je, ni lini mradi wa maji kutoka chanzo cha Mto Zigi kwenda Mkinga na Horohoro utaanza?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Jimbo la Mkinga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza maandalizi ya mpango wa utekelezaji wa mradi wa kutoa maji Mto Zigi kwenye mji wa Kasera ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga, pamoja na Mji wa mpakani wa Horohoro. Kwa sasa taratibu za kumpata Mtaalam Mshauri atakayefanya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa makabrasa zabuni zinaendelea. Matarajio ni Mtaalam Mshauri atakayepatikana atakamilisha kazi hiyo mwezi Septemba, 2019. Ujenzi wa mradi huo unatarajiwa kuanza baada ya kukamilika kwa usanifu.

Mheshimiwa Spika, wakati tunasubiri usanifu wa mradi wa kutoa maji Mto Zigi kukamilika, Serikali imeandaa mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji kwa mpango wa muda mfupi katika Mji wa Horohoro kwa gharama ya kiasi cha shilingi milioni 595. Kazi zitakazotekelezwa ni ulazaji wa bomba, ujenzi wa mtambo mdogo wa kusafisha na kutibu maji, ukarabati wa tanki la maji na ujenzi wa vituo vitano vya kuchotea maji. Mradi huo unatarajiwa kuanza mwezi Juni, 2019 na kukamilika baada ya miezi sita.
MHE. RICHARD M. NDASSA aliuliza:-

Mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoia kwenda katika Miji ya Sumve, Malya hadi Malampaka ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ambao usanifu wake umeshakamilika.

Je, ni lini mradi huo utatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mganga Ndassa, Mbunge wa Jimbo la Sumve kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika Miji ya Sumve, Malya na Malampaka ni ahadi ya Mheshimiwa Rais katika Awamu ya Nne. Tayari Wizara ya Maji kupitia mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mwanza ilinza mchakato wa kufanya upimaji ili kujua ni eneo gani lipo karibu kutoka Ziwa Victoria, ili iwe rahisi kufikisha maji kwenye miji hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 200 kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina ili kuanza na maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa maji katika miji hiyo baada ya gharama halisi kufahamika.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuza:-

Serikali inajitahidi kuwapatia maji wananchi wa Manispaa ya Morogoro. Licha ya jitihada hizo, hadi sasa ipo mitaa ambayo inapata maji kwa mgao na mingine haipati kabisa.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha miundombinu ya Bwawa la Mindu ili wananchi wapate majisafi na salama kwa uhakika muda wote?
NAIBU WAZIRI MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na shirika la maeneleo la Ufaransa AFD inatekeleza mradi wa majisafi na usafi wa mazingira Morogoro iko katika hatua za kumpata mataalam mshauri atakayefanya usanifu wa kina wa bwawa la mindu kwa kwa lengo la kuongeza urefu wa tuta la bwawa ambao utapelekea kuongeka kwa kiwango cha ujazo wa bwawa. Ongezeko la ujazo wa maji katika bwawa utaiwezesha MORUWASA kuongeza kiwango cha ulazishaji wa majisafi hivyo kuondoa mgao katika mitaa inayopata maji kwa mgao. Hatua iliyofikiwa ni kuwa, taarifa ya uchambuzi shortlist report imewasilishwa AFD kwa ajili ya kupata kibali kabla ya kuwapata watalaam washauri makababrasha ya zabuni kwa ajili ya kuwasilisha mapendekezo ya kiufundi na kifedha.

Mheshimiwa Spika, mtaalam mshauri atakapopatikana atafanya usanifu wa kina pamoja na kuandaa vitabu vya zaburi kwa ajili ya manunuzi ya wakandarasi. Matarajio ni kazi ya ujenzi wa mradi huu kuanza katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. CATHERINE N. RUGE aliuliza:-

Mji wa Shirati Wilayani Rorya unakabiliwa na changamoto kubwa ya maji safi na salama licha ya kuwa na umbali wa kilometa 3 tu kutoka Ziwa Victoria. Mji huu ni moja ya Miji Mikongwe ambapo miundombinu yote ya maji ipo tangu enzi za Awamu ya kwanza, lakini hadi leo hakuna maji licha ya kuwepo na Taasisi mbalimbali za Serikali na binafsi zinazohitaji sana huduma ya maji?

Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Shirati juu ya upatikanaji wa maji safi na salama ili kupunguza ukali wa maisha ambapo kwa sasa dumu moja la lita 20 linauzwa mpaka shilingi 100?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Nyakao Ruge, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imepata mkopo wenye masharti nafuu wa dola za Marekani milioni 500 kutoka Serikali ya India kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji katika Miji 28 kwa upande wa Tanzania Bara na mradi mmoja kwa upande wa Zanzibar ambapo Mji wa Shirati umejumuishwa. Utekelezaji wa miradi hiyo umegawanyika katika awamu mbili, awamu ya kwanza ni usanifu na awamu ya pili ni ujenzi wa miradi husika.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa, Serikali ipo katika hatua ya kuwapata Wataalamu washauri watakaofanya usanifu wa kina na uandaaji wa vitabu vya zabuni kwa miradi hiyo ya maji ukiwemo Mji wa Shirati. Ujenzi wa miradi hiyo utaanza katika mwaka wa fedha 2019/2020. Kukamilika kwa miradi hiyo kutamaliza kabisa tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa Mji wa Shirati.
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE aliuliza:-

Wakati wa ziara ya Makamu wa Rais Wananchi wa Halmashauri ya Chalinze walihakikishiwa kuwa maji yataanza kutoka kuanzia tarehe 31 Disemba, 2018 lakini hadi leo hali imekuwa mbaya zaidi kuliko ilivyokuwa mwanzo?

(a) Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Chalinze juu ya hali mbaya ya upatikanaji wa maji?

(b) Je, Waziri yupo tayari twende pamoja Chalinze kufanya Mkutano kuwaambia wananchi juu ya hali ya maji katika Halmashauri yetu na lini sasa wananchi wa Chalinze watarajie maji kuanza kutoka kwenye mabomba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete Mbunge wa Jimbo la Chalinze lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya upatikanaji wa hali ya maji katika Jimbo la Chalinze. Katika kuhakikisha changamoto hiyo inatatuliwa, Serikali imeshakamilisha mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji kwa awamu ya kwanza na Awamu ya II. Kwa sasa Serikali inatekeleza mradi wa maji Chalinze kwa Awamu ya III kwa upanuzi wa mtambo wa kuzalisha maji na mtandao wa usambazaji maji katika maeneo mbalimbali. Katika utekelezaji wa Awamu ya II tayari vituo vya kuchotea maji 96 vimeunganishwa na wananchi wanaendelea kupata maji.

Mheshimiwa Spika, ili kuongeza hali ya upatikanaji wa maji wa wananchi wa Chalinze, Serikali inatekeleza mradi mwingine mkubwa kutoka Mlandizi hadi Chalinze Mboga. Mradi huu utakapokamilika utamaliza kabisa tatizo la maji katika eneo la Chalinze.

Mheshimiwa Spika, nipo tayari kufanya ziara pamoja na Mheshimiwa Mbunge katika Jimbo la Chalinze na kuwaeleza wananchi mipango mbalimbali ya Serikali katika kutatua tatizo la maji.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE aliuliza:-

Kata ya Buhoro Wilaya Kasulu ina shida kubwa ya maji:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapa mradi wa visima vikubwa viwili kwenye kijiji cha Shunga ili kuwasaidia akina mama wanaoteseka?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Augustine Vuma Holle Mbunge wa Kasulu Vijiji kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango wa utekelezaji wa miradi ya maji kwa mwaka 2019/2020, Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu imekiweka kijiji cha Shunga miongoni mwa vijiji vitakavyofanyiwa usanifu wa miradi wa maji. Aidha, mradi mkubwa wa maji kutoka chanzo chake kilichopo eneo la Jeshi la Mutabila kinalenga kuwapatia maji wananchi wa kijiji cha Shunga. Lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wake wote wanapatiwa huduma hii muhimu ya maji safi na salama.
MHE. ESTHER N. MATIKO (K.n.y MHE. JOYCE B. SOKOMBI) aliuliza:-

Mkoa wa Mara unakabiliwa na changamoto za maji safi na salama kwa muda mrefu hasa katika Jimbo la Musoma Vijijini, Wilaya ya Bunda, Jimbo la Serengeti, Butiama na Rorya licha ya kwamba Mkoa huo umezungukwa na Ziwa Victoria:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inasambaza mabomba ya maji katika maeneo yenye ukosefu wa maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joyce Bitta Sokombi kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na washirika wa Maendeleo wanatekeleza mradi wa majisafi wa Mugango, Kiabakari na Butiama kwa gharama za dola za Kimarekani milioni 30.69. kwa sasa Serikali inakamilisha taratibu za manunuzi za kumpata mkandarasi na ujenzi unatarajiwa kuanza katika mwaka huu wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zitakazotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa chanzo cha maji kutoka Ziwa Victoria, ujenzi wa mtambo wa kutibu maji, ujenzi wa matanki ya kuhifadhi maji, ujenzi wa ofisi ya mamlaka, ujenzi wa vituo vya kuchotea maji na ujenzi wa mabirika ya kunyweshea mifugo. Mradi huu unatarajiwa kujengwa ndani ya kipindi cha miaka miwili hadi kukamilika na utahudumia watu wapatao 164,924 katika Miji ya Mugango, Kiabakari, Butiama pamoja na vijiji 13 vilivyopo katika halmashauri ya Musoma Vijijini pamoja na Butiama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maji ina mpango wa muda mrefu kwa wananchi waishio kwenye vijiji arobaini vilivyopo kandokando ya Ziwa Victoria kwenye Mkoa wa Mara ili kuhakikisha wanapata maji safi na salama. Wizara imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na hatua inayofuata ni kukamilisha usanifu wa kina wa miradi ya maji kwa ajili ya vijiji vyote 40.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali imefanya makubaliano na mtaalam mshauri ya kufanya utafiti na usanifu kuangalia uwezekano wa kuwapatia wananchi wengine zaidi huduma hii muhimu ya maji kutoka Ziwa Victoria.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Jimbo la Bunda hususan Kata saba za Mugeta, Mihinyo, Kitale, Nyamuswa, Nyamang’uta, Hunyari na Salama zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa maji ya kunywa; na Serikali ilishaliona hilo na kuwapeleka wataalam wake kufanya survey katika kata hizo:-

Je, baada ya survey hiyo nini kimeamuliwa na Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutatua tatizo la uhaba wa maji katika kata saba zilizopo Jimbo la Bunda, wataalam kutoka Wizara ya Maji kwa kushirikiana na wataalam kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Bunda walifanya upimaji (survey) katika vijiji 23 vilivyopo katika kata hizo. Matokeo ya upimaji yalionyesha ni maeneo 10 tu yenye uwezo wa kuhifadhi maji kati ya mita za ujazo 84,794 hadi 354,604. Maeneo hayo ni ya vijiji vya Tingirima, Salama A, Marembeka, Kambumbu, Bigegu, Mahanga, Mihingo, Nyaburundu, Rakana na Manchimweru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020, Wizara imeweka mabwawa matano katika mpango ili kuanza utekelezaji wa mabwawa hayo ikiwemo Tingirima na Salama A. Aidha, kwa maeneo ambayo hayakufanikiwa kupata vyanzo hivyo vya mabwawa, Serikali itaendelea na tafiti za kuangalia uwezekano wa kupata maji chini ya ardhi au kutumia chanzo cha Ziwa Victoria.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI (K.n.y. MHE. ESTER A. BULAYA) aliuliza:-

Jimbo la Bunda Mjini ni miongoni mwa majimbo yanayokabiliwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama?

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha maeneo yote yanayopitiwa na mradi mkubwa wa maji - Nyahebu hasa vijiji vya Nyatare yananufaika na mradi huo?

(b) Kwa kuzingatia kwamba siyo kila mwananchi atakuwa na uwezo wa kuvuta maji nyumbani kwake kutokana na ukubwa wa gharama katika utekelezaji wa mradi tajwa hapo juu; je, Serikali inatarajia kujenga vituo vingapi vya maji?

(c) Je, ni nini Serikali itatekeleza ahadi yake ya usambazaji wa mabomba awamu ya pili katika Kata za Manyamanyama, Nyasura, Kabalimu, Bundastoo, Nyamakokoto, Balili na Bunda Mjini?
NAIBU WAZIRI MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Amos Bulaya, Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaunganisha vijiji vya Nyabeho, Guta na Tairo na mradi mkubwa ambapo wananchi wa vijiji hivyo wanapata huduma ya maji kupitia mradi huo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa kijiji cha Kinyambwiga Serikali inaendelea na ujenzi wa kuunganisha kijiji hicho na Mradi mkubwa kwa gharama ya shilingi milioni 923.3 na hadi kufikia mwezi Machi, 2019 ujenzi huo umekamilika kwa asilimia 70. Aidha, kijiji cha Nyantare kitaunganishwa na mradi huo katika mwaka wa fedha 2019/ 2020.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilipanga kujenga vituo 42 vya kuchotea maji katika maeneo mbalimbali ya Mji wa Bunda ambapo kwa sasa imeshakamilisha ujenzi wa vituo 22, aidha, Serikali inaendelea na ujenzi wa vituo zaidi vya kuchotea maji kwa lengo la kusogeza huduma ya maji kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mradi wa usambazaji wa maji ambapo hadi kufikia mwezi Machi, 2019 jumla la km 32 zimelazwa katika maeneo mbalimbali ya kata alizozitaja Mheshimiwa Mbunge. Aidha, Serikali itaendelea na kazi ya upanuzi wa mtandao wa usambazaji ili kuhakikisha wananchi wote wa Jimbo la Bunda wanapata huduma ya maji safi. (Makofi)
MHE. JEROME D. BWANAUSI aliuliza:-

Wananchi wengi wa Vijiji vya Mieji, Utimbe, Naliongolo, Mtolya, Geuza na Mchoti wamekuwa wakiliwa na mamba na wengine kujeruhiwa vibaya hasa wanapokwenda kuchota maji katika Mto Ruvuma kutokana na ukosefu wa maji katika maeneo yao.

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kuchimba visima vya maji katika vijiji hivyo ili kunusuru wananchi wanaouawa na kujeruhiwa na mambo wnapofuata maji katika mto huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerome Dismas Bwanausi Mbunge wa Lulindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wananchi wa vijiji vya Miesi, Utimbe, Naliongolo, Mtolya, Geuza na Mchoti wana shida ya kupata majisafi na salama na sehemu pekee ya kupata maji ya matumizi ya nyumbani ni kutoka Mto Ruvuma. Hata hivyo kutokana na umbali uliopo kati ya vijiji hivyo inapelekea gharama ya kuchukua maji katika Mto Ruvuma kuwa kubwa ukilinganisha na gharama ya kuchimba visima.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2019/2020 Halmashauri ya Masasi inategemea kuingia mkataba wa kuchimba visima na Wakala wa uchimbaji visima na ujenzi wa mabwawa (DDCA) katika vijiji 26 kwa gharama ya shilingi milioni 579.

Mheshimiwa Spika, rasimu ya Mkataba wa uchimbaji wa visima katika vijiji 26 umewasilishwa Wizarani na tayari kibali kimetolewa kwa ajili ya kuendelea na utekelezaji wa mradi huo.
MHE. MUSA R. NTIMIZI aliuliza:-

Serikali ina mpango wa kuleta maji katika Mkoa wa Tabora toka Ziwa Victoria lakini Jimbo la Igalula halipo katika ratiba hiyo.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza vijiji vya Jimbo la Igalula katika mradi huo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musa Rashid Ntimizi, Mbunge wa Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mradi wa kutoa maji Ziwa Victoria kwenda katika miji ya Tabora, Igunga na Nzega pamoja na vijiji zaidi ya 80 vilivyopo umbali wa kilometa 12 kila upande kutoka bomba kuu. Vijiji vilivyopo katika Jimbo la Igalula vipo umbali wa zaidi ya kilometa 30 toka linapopita bomba kuu, hivyo kushindwa kuingizwa kwenye mradi huu.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali imeanza kutekeleza miradi mbalimbali katika Jimbo la Igalula kwa kutumia vyanzo vya maji vingine ambapo kwa sasa usanifu unaendelea katika Kata za Tura, Nsololo na Loya. Ujenzi wa miradi hii, inategemewa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2019/2020.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza:-

Mradi wa Maji wa Mto Mbwinji upo kwenye chanzo chenye maji ya kutosha, ambapo bomba la mradi linaloelekea Nachingwea limepita kwenye vijiji vyenye matatizo makubwa ya maji.

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha vijiji vyote vinavyopitiwa na bomba la maji vinapata huduma hiyo?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuwahakikisha wananchi wa Ndanda kuwa zahanati na vituo vya afya vitaunganishwa na huduma hii muhimu ya upatikanaji wa maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Ndanda lenye sehemu (a) (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Safi wa Masasi – Nachingwea licha ya kuhudumia miji ya Masasi na Nachingwea, pia unatoa huduma ya maji katika vijiji vilivyo kandokando ya mabomba makuu yatokayo kwenye chanzo cha Mbwinji kuelekea katika miji hiyo. Hadi sasa jumla ya vijiji 30 katika Wilaya ya Masasi, Nachingwea na Ruangwa vimeshaunganishwa na mradi huo. Serikali kupitia Mamlaka ya Maji Safi Nachingwea (MANAWASA) itaendelea kuunganisha vijiji vyote vilivyopo kandokando ya bomba kuu ili kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshaanza kuunganisha zahanati mbalimbali na huduma za maji ambapo hadi sasa imeshaunganisha zahanati za Nangoo, Chisegu na Chikundi zilizopo Wilaya ya Masasi. Aidha, kwa zahanati za Naipanga na Mkotokuyana Wilaya ya Nachingwea, zahanati za Nandanga na Mbecha Wilaya ya Ruangwa zinapata huduma za maji katika vituo vya kuchotea maji vilivyojengwa karibu. Serikali itaendelea kuhakikisha zahanati zote pamoja na vituo vya afya vinaunganishwa na huduma ya maji.
MHE. ALBERT O. NTABALIBA aliuliza:-

Ni lini Serikali itavipatia maji vijiji vya Rusaba, Kilelema, Migongo, Nyaruboza na Kibwigwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Albert Obama, Mbunge wa Buhigwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya hali ya huduma ya maji inayoikabili Halmashauri ya Buhigwe kwa vijiji vya Rusaba, Kilelema, Migongo, Nyaruboza na Kibwigwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika vijiji vya Kilelema na Migongo mkandarasi wa kujenga miundombinu ya miradi ya maji katika vijiji hivyo amepatikana. Aidha, mabomba yatakayolazwa katika mradi huo tayari yameagizwa na mara yatakapoasili yatalazwa katika mtandao wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika vijiji vya Rusaba, Nyaruboza na Kibwigwa, vimewekwa katika Mpango wa Utekelezaji katika Awamu ya Pili ya Programu ya Maji ambapo vitatekelezwa katika mwaka 2020/21.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2019/ 2020 Halmashauri ya Buhigwe imetengewa jumla ya shilingi bilioni 1.15 ili kuhakikisha miradi ya maji inakamilika na wananchi wanapata huduma ya maji.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:-

Matatizo ya maji katika Jimbo la Rufiji ni ya muda mrefu kwenye maeneo kadhaa hususan Kata ya Ngarambe maji hupatikana kwa umbali zaidi ya kilometa 7 - 10 na kwa kuwa Serikali sasa inaleta sera ya Maji ndani ya mita 400:-

Je, ni lini Serikali itatua kero ya maji katika Kata ya Ngarambe, Mbwala, Chumbi, Muholo, Kipugila na maeneo mbalimbali ya Tarafa ya Ikwiriri hata kwa kuchimba visima?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya huduma ya maji katika Halmashauri ya Rufiji na kwa sasa tayari baadhi ya kata hizo zimeanza kupewa kipaumbele kwa kujengewa miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Mbwala kuna mradi wa kisima kirefu ambao unatumia teknolojia ya dizeli. Mradi huo kwa sasa una changamoto ya uendeshaji kwani wananchi wanatumia gharama kubwa kwa kununua mafuta ya uendeshaji wa mitambo ya mradi huo. Halmashauri inaendelea na taratibu za kutumia teknolojia ya umeme wa REA ambao tayari umeshafika katika kata hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Chumbi vimechimbwa visima viwili ambapo kwa sasa vipo katika hatua ya usanifu wa miradi. Kata ya Muholo imewekwa katika utekelezaji wa miradi ya awamu ya pili ambapo kwa sasa usanifu katika visima viwili umekamilika. Wizara imeshatoa kibali kwa ujenzi wa miundombinu kwani miundombinu ya awali ilichakaa na haifai tena kwa mradi. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Halmashauri ya Rufiji imetengewa jumla ya shilingi milioni 871.98 kwa ajili ya kuendelea kukamilisha miradi ya zamani ya kujenga miradi mipya.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza:-

Mradi wa Maji wa Bwawani umekuwa ukisuasua kujengwa ikiwemo kuzungushiwa uzio:-

Je, ni lini mradi huo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba wa ujenzi wa mradi wa kuboresha huduma ya maji kwenye Mji wa Makambako ulisainiwa tarehe 23/05/2017 kati ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Iringa (IRUWASA) na Kampuni ya Ujenzi inayoitwa Building Water and Earth Works Ltd ya Jijini Dar es Salaam kwa gharama ya shilingi bilioni 1,568 ikiwa ni pamoja na kodi ya ongezeko la thamani (VAT). Kazi ya ujenzi ilianza tarehe 08/06/2017 na kwa mujibu wa mkataba, kazi hii ilitakiwa kukamilika tarehe 08/02/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulijitokeza kazi ya ziada ya ujenzi wa uzio kuzunguka chanzo cha maji cha bwawani ili kuzuia uchafuzi unaofanyika kwenye chanzo hicho. Kazi hii imeongeza muda wa kukamilisha kazi zilizopangwa kwa mujibu wa mkataba hadi tarehe 30/06/2019. Kwa sasa uzalishaji wa maji katika chanzo hicho unaendelea na tayari mradi huo unatoa huduma kwa wananchi. Kazi zilizobaki zitaendelea kukamlishwa huku wananchi wakiendelea kupata huduma ya maji.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA (K.n.y MHE. DAVID E. SILINDE) aliuliza:-

Je, ni upi mpango wa sasa wa kutatua kero ya maji katika Jimbo la Momba?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, Kwa niaba ya Mheshimwa Maziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa sasa wa Serikali wa kutatua kero ya maji katika Jimbo la Momba ni kupitia utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP) ambayo inatekelezwa pia katika Halmashauri zote nchini. Programu hiyo imelenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu ya majisafi na salama.

Mheshimiwa Spika, kupitia pragramu hiyo, tayari katika Wilaya ya Momba Serikali imekamilsha miradi ya maji mitano katika vijiji vya Namtambala, Itumbula, Iyendwe, Mnyuzi na Chilulumo ambapo jumla ya wananchi 20,271 wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, Halmashauri ya Wilaya ya Momba imetengewa kiasi cha Sh.1,744,000,000 kwa ajili ya uchimbaji wa visima, usanifu na ujenzi wa miundombinu ya maji. Utekelezaji wa miradi hiyo uko katika hatua mbalimbali ambapo mradi wa maji katika Kijiji cha Tindingoma, mkandarasi amesaini mkataba kwa ajili ya ujenzi; Mradi wa maji katika Kijiji cha Kitete upo kwenye hatua za manunuzi; na kwa ajili ya kumpata mkandarasi wa ujenzi wa mradi katika Kijiji cha Ikana upo kwenye hatua ya usanifu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hatua hizo zilizochukuliwa, Serikali pia ipo katika hatua ya manunuzi ya kumpata makandarasi wa kupima na kuchimba visima katika vijiji saba (7) vya Mpapa, Samang’ombe, Kasinde, Namsinde, Chole, Nkangamo na Itelefya. Vilevile, mkandarasi huyo atafanya usanifu wa mradi wa maji utakaotumia chanzo cha Mto Momba kwa kuhudumia vijiji 21 vya Ivuna, Lwate, Mkomba, Ntungwa, Kalungu, Sante, Tontela, Kaonga, Nsanzya, Chuo, Namsinde I, Kasanu, Masanyinta, Senga, Mweneemba, Makamba, Naming’ongo, Yala, Muuyu, Usoche na Makao Makuu ya Wilaya ya Momba.
MHE. HAWA A. GHASIA aliuliza:-

Tatizo la maji Mkoani Mtwara limeendelea kuwa kero kubwa kwa wananchi wa Mkoa huo:-

(a) Je, mradi wa kutoa maji mto Ruvuma hadi Mtwara Manispaa umefikia hatua gani?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za ukarabati wa Mradi wa Maji wa Mbuo Nkunwa?

(c) Je, ni nini hatma ya Mradi wa Maji Makonde?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini, lenye Sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha upembuzi yakinifu wa mradi wa kutoa maji katika chanzo cha maji cha Mto Ruvuma kwa ajili ya wakazi wa Mkoa wa Mtwara. Kwa sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuajiri mtaalam atakayefanya usanifu wa kina na kuandaa makabrasha kwa ajili ya kuanza utekelezaji katika mwaka wa fedha 2020/2021. Mradi huu ni mkubwa, ukitekelezwa utakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa Mkoa wa Mtwara.

(b) Mheshimiwa Spika, ukarabati wa mradi wa maji Mbuo – Nkunwa unaendelea kufanyika na Mkandarasi anaendelea na kazi. Mpaka sasa bomba la njia kuu lenye urefu wa kilomita 3.6 limelazwa na wananchi wanaendelea kupata huduma ya maji.

Pia mkandarasi amechimba kisima kingine kipya ili kuongeza kiasi cha maji. Kazi ya kufunga miundombinu ya bomba la mtandao wa maji inaendelea. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Aprili, 2020. Usimamizi wa mradi huu unafanywa na wataalam wa ndani (force account) wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mtwara (MTUWASA).

(c) Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mradi wa Makonde, Serikali imepanga kufanya ukarabati kwa awamu. Awamu ya kwanza ya ukarabati inaendelea ambapo tayari njia ya bomba kuu yenye urefu wa kilomita 17 kutoka chanzo cha maji Mitema hadi Mjini Newala imekamilika.

Mheshimiwa Spika, kazi ya ufungaji wa pampu inaendelea ili majaribio ya mradi yafanyike kwa ajili ya Mji wa Newala. Aidha, katika awamu hii upo mpango wa kuongeza njia nyingine kubwa kutokea Mitema hadi eneo la Nambunga ambapo tenki lenye uwezo wa lita milioni tano litajengwa na maji yatasambazwa katika Mji wa Newala na vijiji jirani. Awamu ya pili itahusisha ukarabati wa mtandao wa mabomba katika eneo la Tandahimba ili kutoa huduma ya maji ya uhakika.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia maji wananchi walio katika Vijiji ambavyo havifikiwi na Mradi wa Maji kutoka Ziwa Victoria katika Jimbo la Tabora Kaskazini?
WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Tabora Kaskazini lina kata 19 na vijiji 82. Katika utekelezaji wa mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika Miji ya Nzega, Igunga na Tabora jumla ya vijiji 20 vya Jimbo la Tabora Kaskazini ambavyo ni Ibushi, Igoko, Isikizya, Ikonola, Ikonola, Mswa, Itobela, Ibelamilundi, Isenegezya, Mtakuja, Majengo, Kalemela, Saw Mill, Imalampaka, Magiri, Kinyamwe, Lunguya, Upuge, Kasenga na Mhogwe vimenufaika na mradi. Aidha, Serikali imekamilisha utekelezaji wa miradi mitatu ya mtandao wa bomba inayonufaisha vijiji vinne vya Kilungu, Milumba, Migungumalo na Ishihimulwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali iko kwenye hatua za awali za utekelezaji wa miradi sita itakayonufaisha vijiji kumi na mbili vya Makazi, Ugowola, Ndono, Mbiti, Kalola, Ufuluma, Nzubuka, Izugawima, Ibiri, Mayombo, Nsimbo na Kagera. Katika Mpango wa bajeti ya fedha 2021/2022, Serikali imepanga kutekeleza miradi mitano itakayonufaisha vijiji vinane vya Ikongolo, Kanyenye, Kiwembe, Kongo na miji 28 kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 500 kutoka Benki ya Exim India ambao utanufaisha vijiji 14 na hivyo kufanya jumla ya vijiji 58 vya Jimbo la Tabora Kaskazini kupata huduma ya maji.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa kujenga miundombinu ya maji katika vijiji vya Kipunda, Minyughe, Ighombwe, Makungu, Mpetu, Magungumka na Mnang’ana?
WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya hali ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Jimbo la Singida Magharibi. Ili kuendelea kutatua changamoto hiyo, Serikali imekamilisha upatikanaji wa vyanzo vya maji kwa kuchimba visima virefu katika Vijiji vya Kipunda, Minyughe, Ighombwe, Makungu, Mpetu, Magungumka na Mnang’ana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uendelezaji wa visima hivyo kwa kujenga miundombinu ya usambazaji utaanza mwaka wa fedha 2021/2022 ambapo kazi zitakazofanyika ni pamoja ununuzi na ufungaji wa pampu saba, ujenzi wa nyumba za mashine saba, matanki ya kuhifadhi maji saba yenye ukubwa lita 90,000 na 100,000 na ununuzi na ulazaji wa mabomba ya usambazaji maji umbali wa kilometa 85.9 na ujenzi wa vituo vya kuchotea maji 79. Pia, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepanga kutekeleza miradi minne ya ujenzi wa miundombinu ya maji katika vijiji vya Irisya, Iglansoni, Ihanja na Kaugeri vilivyopo katika Jimbo Singida Magharibi. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kusambaza maji kutoka Mradi wa Maji Mhangu – Ilogi katika Kata za Lunguya, Ikinda, Shilela, Sogese na Mega katika Halmashauri ya Msalala?
WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Msalala, Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imeendelea na utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Mhangu – Ilogi awamu ya kwanza ambayo ilihusisha ujenzi wa bomba kuu kutoka Mhangu hadi Ilogi umbali wa kilometa 56 kwa gharama ya shilingi bilioni 13.86 na kazi hii inatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi huu kwa awamu ya pili ambayo itahusisha usanifu wa miundombinu ya usambazaji maji na ujenzi wa miundombinu hiyo katika kata zote tano ambapo mradi unatarajiwa kuanza mwanzoni mwa mwaka 2022.
MHE. MASACHE N. KASAKA K.n.y. MHE. FRANCIS L. MTEGA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Mradi wa Maji Ruduga – Mawindi ili kuwatua ndoo kichwani akina mama wa Mbarali?
WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha wananchi wa Wilaya ya Mbarali wanapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza, Serikali ilianza ujenzi wa Mradi wa Maji wa Luduga – Mawindi kwa lengo la kuhudumia vijiji sita vya Kangaga, Mkandami, Itipingi, Manienga na Ipwani kwa gharama ya jumla ya shilingi bilioni. 9.66. Utekelezaji wa mradi huo umepangwa kwa awamu (lots) tano. Kazi zilizopangwa kutekelezwa kwa awamu zote ni ujenzi wa banio la maji, mtandao wa bomba jumla ya kilometa 139, matanki sita yenye ujazo wa lita 150,000 moja, lita 100,000 matatu na lita 75,000 mawili na vituo vya kuchotea maji 119.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi sasa kazi zilizofanyika ni pamoja na ujenzi wa banio la maji, mtandao wa bomba jumla ya kilometa 54 na tanki la kuhifadhia maji la lita 150,000, ujenzi wa vituo vya kuchotea maji 12. Kwa kazi zilizokamilika wananchi wa Kijiji cha Kangaga wameanza kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 utekelezaji wa mradi utakamilika na huduma ya maji itapatikana katika vijiji vyote na kunufaisha wananchi zaidi ya 26,000. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza upembuzi yakinifu na ujenzi wa miundombinu ya maji katika Ziwa Madunga ili kutatua tatizo sugu la maji katika Kata ambazo hazina maji Jimbo la Babati Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa Babati Vijijini ni asilimia 74. Kwa lengo la kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama na yenye kutosheleza kwa wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Serikali inaendelea na utafiti wa ubora na uwingi wa maji katika chanzo cha Ziwa Madunga. Utafiti huo unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2021 na usanifu wa miundombinu ya maji utakamilika katika robo ya pili ya mwaka wa fedha 2021/2022.
MHE. VINCENT P. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza mradi wa maji wa Mji Mdogo wa Chala ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni za mwaka 2020?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vicent Paul Mbogo Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji mdogo wa Chala unapata maji kutoka Mto Kauzike na Bwawa la Ntanganyika na hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika Mji huo ni asilimia 56. Aidha, katika kuhakikisha huduma ya maji katika mji wa Chala inaboreshwa mwaka 2020/2021 ulitekelezwa mradi wa maji ambao umehusisha kuchimba kisima kirefu chenye uwezo wa kuzalisha lita 153,600 kwa siku na kiasi hiki kimeongeza upatikanaji wa maji zaidi ya lita 300,000 kwa siku. Hivyo kazi itakayofanyika kuanzia mwezi Julai, 2021 ni ujenzi wa miundombinu ya usambazaji maji, ujenzi wa nyumba ya mtambo wa maji, ufungaji wa pampu na ulazaji wa bomba mita 500 kwenda kwenye tanki lililopo la lita 150,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji wakati wote, hivyo mpango wa muda mrefu katika mji wa Chala ni kutumia mabwawa madogo na ya ukubwa wa kati ambapo kwa sasa utafiti wa kubainisha maeneo yanayofaa kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa mawili (2) katika Mji Mdogo wa Chala unaendelea na unatarajiwa kukamilika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2021/2022.
MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kusafisha na kuongeza kina cha Bwawa la Maji Lukuledi-Masasi linalohudumia Vijiji vya Lukuledi, Nambawala, Mraushi, Mwangawaleo na Ndomoni?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jukumu la Serikali ni kuhakikisha maeneo mbalimbali yanapata huduma ya maji ya uhakika na kipaumbele ni maji kwa matumizi ya nyumbani ambapo Vijiji vya Lukuledi, Ndomoni na Nambawala vinapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Katika mwaka wa fedha 2021/2022 kazi ya ujenzi wa miundombinu ya kufikisha maji Kijiji cha Mraushi pamoja na Kitongoji cha Mwangawaleo, utekelezaji unaendelea ambapo utahusisha ulazaji wa bomba lenye urefu wa kilometa sita, vituo vya kuchotea maji 16 na ujenzi wa tanki la lita 100,000 kuongeza upatikanaji wa maji katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Vijiji vya Lukuledi, Nambawala, Mraushi na Ndomoni wanatumia maji ya Bwawa la Lukuledi. Hivyo, kutokana na umuhimu huo katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itakamilisha usanifu na kuanza ukarabati wa bwawa hilo ili liwe na uwezo wa kuhifadhi maji mengi ya kukidhi mahitaji ya shughuli hizo za maendeleo.
MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo la maji katika Mji wa Vwawa?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya maji ya Mji Vwawa ni zaidi ya lita milioni 10 kwa siku ambapo kwa sasa hali ya upatikanaji wa huduma ya maji ni asilimia 43.2.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mipango ya muda mfupi na muda mrefu ili kuboresha huduma ya maji safi na salama katika Mji wa Vwawa ambapo katika mpango wa muda mfupi mwaka 2020/2021, Wizara imechimba visima virefu vitatu vyenye uwezo wa kuzalisha maji lita 600,000 kwa siku. Ujenzi wa miundombinu ya usambazaji maji ya visima hivyo utafanyika ndani ya mwaka wa fedha 2021/2022 na kuongeza huduma ya upatikanaji wa maji kwa wakazi wa Mji wa Vwawa kufikia asilimia 70.

Mheshimiwa Spika, katika mpango wa muda mrefu wa kuboresha huduma maji safi, salama na yenye kutosheleza kwa wakati wa mji huo Serikali imepanga kujenga mradi kupitia chanzo cha maji cha Mto Bupigu uliopo Wilaya ya Ileje wenye uwezo wa kuzalisha maji kiasi cha lita milioni 73 kwa siku. Mtaalam Mshauri kwa ajili ya kufanya Usanifu wa Kina yaani detailed design wa mradi huu anatarajiwa kupatikana katika robo ya kwanza ya mwaka 2021/2022 mradi huu utanufaisha Miji ya Vwawa, Mlowo na Tunduma katika Mkoa wa Songwe.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza: -

(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa kupeleka maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Kigwa, Goweko, Igalula na Nsololo?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa uchimbaji wa mabwawa katika Kata za Mmale, Miswaki, Lutende na Kizengi ili kupunguza changamoto ya upatikanaji wa maji katika maeneo hayo?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Igalula lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imepanga kuboresha huduma ya maji kwenye Kata za Kigwa, Goweko, Igalula na Nsololo kupitia bomba kuu linalotoa maji Ziwa Victoria kupeleka Miji ya Nzega, Igunga na Tabora.

Kazi zitakazofanyika ni pamoja na ujenzi wa tenki lenye ujazo wa lita 1,000,000 na ulazaji wa mabomba yenye urefu wa kilometa 122. Mradi huu unatarajiwa kukamilika kabla mwezi Juni, 2022 na utanufaisha wananchi wapatao 123,764 kwa kupata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepanga katika robo ya pili ya mwaka wa fedha 2021/2022 kukamilisha usanifu wa ujenzi wa bwawa katika Kata ya Kizengi na wakandarasi watapatikana mwezi Machi, 2022 kwa ajili ya ujenzi wa bwawa hilo ambapo wananchi wa Kata za Kizenga, Mmale, Miswaki na Lutende zaidi ya 60,000 watanufaika.
MHE. DKT CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza vituo vya kuchotea maji katika Mji Mdogo wa Gairo?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi wa Mji wa Gairo kwa sasa ni wastani wa asilimia 75. Katika Mwaka wa Fedha 2020/2021 Serikali imeendelea kuboresha huduma ya maji kwa wananchi kwa kufanya upanuzi wa mtandao wa maji katika Mji wa Gairo ambapo kazi zilizofanyika ni pamoja na ulazaji wa mabomba ya kusambaza maji umbali wa kilometa nane na ujenzi wa vituo vya kuchotea maji vitano, hivyo vituo hivyo vya kuchotea maji kuongezeka kutoka vituo 70 na kufikia 75.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bajeti ya Mwaka 2021/2022, Serikali imepanga kuendelea kuboresha huduma ya maji safi na salama katika Mji wa Gairo ambapo kazi zitakazofanyika ni pamoja na ulazaji wa mabomba yenye urefu wa kilometa 21.8 ili kupeleka maji majumbani na ujenzi wa vituo vya kuchotea maji 40. Aidha, kwa lengo la kuongeza uzalishaji maji, Serikali imepanga kutekeleza Mradi wa Maji wa Chagongwe utakaonufaisha maeneo ya Mji wa Gairo na vijiji vya pembezoni.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA K.n.y. MHE. CHARLES M. KAJEGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza dhamira yake ya kuwatua Wanawake ndoo kichwani kwa kuwasogezea huduma za maji safi na salama karibu na makazi yao katika Jimbo la Mwibara?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini nitumie nafasi hii kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutuamini sisi Wizara ya Maji. Nataka niahidi Waheshimiwa Wabunge na watanzania mimi Jumaa Aweso na timu nzima ya Wizara ya Maji, hatutokuwa kikwazo kwa watanzania kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya timu nzima ya Menejimenti ya Wizara ya Maji tunatoa pongezi kwa Mheshimiwa Spika Dkt. Tulia Ackson kwa kuaminiwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sisi Wizara ya Maji tutatoa ushirikiano wa dhati katika kuhakikisha tunafanikisha Bunge hili letu tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Charles Muguta Kajenge, Mbunge wa Mwibara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu la Serikali ni kuhakikisha kuwa upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi ni ya uhakika na endelevu. Kwa sasa, upatikanaji wa huduma ya maji katika Wilaya ya Bunda ambapo Jimbo la Mwibara lipo wastani wa asilimia 69 kupitia visima virefu na vifupi 237 vya pampu za mkono, chemchemi moja na skimu za mtandao wa bomba tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali inaendelea na mpango wa muda mfupi wa kuboresha huduma ya maji katika Jimbo la Mwibara kwa kutekeleza miradi mipya ya Buzimbwe, Bulendabufwe, Igundu, upanuzi wa mradi wa maji Iramba kwenda vijiji vya Mugara, Nyarugoma na Muhura. Kazi zinazofanyika kwa miradi mipya ni pamoja na ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji lenye ujazo wa lita 135,000, ujenzi wa vituo 28 vya kuchotea maji, ujenzi wa ofisi moja ya jumuiya ya watumiaji maji na ujenzi wa nyumba ya mitambo (pump house).

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kazi zinazofanyika kwa mradi wa upanuzi ni pamoja na ulazaji wa mabomba umbali wa Kilometa 18.6, ununuzi na ufungaji wa pampu mpya (surface pump). Miradi hii kwa sasa imefikia wastani wa asilimia 15 za utekelezaji na inatarajia kukamilika mwezi Juni, 2022. Kukamilika kwa miradi hii kutaboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa Wilaya ya Bunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kuwa changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji katika Wilaya ya Bunda inapatiwa ufumbuzi wa kudumu, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 itakamilisha usanifu wa mradi wa maji wa Kisorya kupitia chanzo cha maji cha Ziwa Vicktoria. Mradi huo umepangwa kuhudumia vijiji 12 vya Sunsi, Masahunga, Kisorya, Nambubi, Mwitende, Nansimo, Nambaza, Busambara, Mwibara, Kibara A, Kibara B na Kasahanga. Ujenzi wa mradi unatarajiwa kutekelezwa kupitia bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 baada ya usanifu kukamilika. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA K.n.y. MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawapatia maji wananchi wa Vijiji vya Kata za Imasela, Ilola, Lyamidati, Lyabukande na Nyida ambao wapo ndani ya Kilometa 12 kutoka katika mtandao wa maji ya Ziwa Victoria?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa huduma ya maji katika Kata za Imasela, Ilola, Lyamidati, Lyabukande na Nyida zenye jumla ya vijiji 21 ni wastani wa asilimia 49.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kuwa Vijiji vya Kata za Imasela, Ilola, Lyamidati, Lyabukande na Nyida vilivyopo ndani ya Kilometa 12 vinapata huduma ya maji kutoka katika mtandao wa maji ya Ziwa Victoria, Serikali imepanga kupeleka maji Kata ya Imasela kupitia awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa Tinde - Shelui. Utekelezaji wa mradi huo, ulianza mwezi Agosti, 2021 na kwa sasa, umefikia asilimia 15. Natarajia kuwa ifikapo mwezi Agosti, 2022 mradi utakuwa umekamilika.

Aidha, Serikali imepanga kufanya usanifu wa mradi wa maji wa Kata za Ilola, Nyida na Lyamidati ambao utaanza mwishoni mwa mwezi Februari, 2022 na kukamilika mwezi Juni, 2022. Ujenzi wa mradi huu unatarajiwa kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Kata ya Lyabukande, usanifu umekamilika kwa ajili ya upanuzi wa mradi wa maji wa Ziwa Victoria katika vijiji vya Mwashagi na Buzinza. Ujenzi wa mradi katika Kijiji cha Mwashagi Kata ya Lyabukande utatekelezwa ndani ya mwaka huu wa fedha kwa kutumia fedha za UVIKO – 19, ambapo Mkataba wa ujenzi ulisainiwa tarehe 07 Januari, 2022 na unatarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwezi Juni,2022. Kwa upande wa Kijiji cha Buzinza, utekelezaji wa mradi utaingizwa katika bajeti ya 2022/2023.
MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: -

Je, ni programu zipi zinatekelezwa kuvuna maji ya mvua na asilimia ngapi ya Wananchi hutumia huduma hiyo?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilibuni Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP) inayotekelezwa nchini kote kuanzia mwaka 2006 hadi 2025. Programu hiyo inatekelezwa kupitia Programu ndogo tatu ambapo pamoja na mambo mengine, programu hizo zinazingatia uvunaji maji ya mvua kwa kuelekeza ujenzi wa mabwawa makubwa, ya kati na madogo na pia, uvunaji wa maji ya mvua kwa kutumia mapaa ya nyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia programu hizo, mabwawa yamejengwa na kukarabatiwa kwenye maeneo mbalimbali nchini na katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali inaendelea na ujenzi na ukarabati wa mabwawa ya ukubwa wa kati na madogo katika wilaya 16, ujenzi wa mabwawa ya kimkakati ya Farkwa na Kidunda na usanifu wa ujenzi wa mabwawa katika Wilaya 24. Aidha, Serikali ilitoa mwongozo wa Uvunaji wa Maji ya Mvua kupitia mapaa ya nyumba kwa watu binafsi na taasisi za Umma na kwa sasa miundombinu hiyo inaonekana katika maeneo mbalimbali nchini. Serikali itatafiti kufahamu ukubwa wa matumizi ya teknolojia hiyo nchini.
MHE. ALEXANDER P. MNYETI K.n.y. MHE. DAVID M. KIHENZILE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka maji katika Kata ya Mwabuki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alexander Pastory Mnyeti Mbunge wa Jimbo la Misungwi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kata ya Mwabuki ina jumla ya vijiji sita vya Lubuga, Mhungwe, Mabuki, Mwagagala, Mwanangwa na Ndinga. Kwa sasa vijiji hivyo vinapata huduma ya maji kupitia visima vya pampu za mkono ambapo hali ya huduma ya maji ni asilimia 39.

Mheshimiwa Spika, katika kuboresha huduma ya maji Kata ya Mwabuki katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imekamilisha usanifu wa mradi wa maji kutoka bomba kuu la KASHWASA kupeleka katika vijiji vyote vya Kata ya Mwabuki. Kwa sasa taratibu za manunuzi zinaendelea na ujenzi unatarajiwa kuanza mwezi Desemba, 2022 na kukamilika mwezi Desemba, 2023. Kukamilika kwa mradi huo kutaongeza huduma ya upatikanaji wa maji kutoka asilimia 39 hadi kufikia asilimia 100.
MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kumaliza tatizo la maji safi na salama Wilaya za Newala, Tandahimba na Nanyumbu Mkoani Mtwara?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji 26 ambapo miradi 14 imekamilika na miradi 12 ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Aidha, Serikali imeanza ujenzi wa mradi wa maji wa miji 28, ambapo Mkoa wa Mtwara miradi inayotekelezwa ni mradi wa maji Makonde na Nanyumbu. Utekelezaji huu unatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2024 na utanufaisha wananchi zaidi ya 500,000 wa Wilaya za Newala, Tandahimba na Nanyumbu.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza: -

Je, ni lini Miradi ya maji Halmashauri ya Msalala itaanza kutekelezwa baada ya Serikali kutenga Shilingi bilioni 4.8 kwa ajili ya miradi hiyo?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi Mbunge wa Jimbo la Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi ya maji katika Halmashauri ya Msalala. Katika mwaka wa fedha 2021/2022, jumla ya miradi mitano ilikamilika. Katika mwaka 2022/2023, Serikali inaendelea na ujenzi wa miradi 12 ambapo miradi miwili imekamilika na miradi 10 ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, aidha, utekelezaji wa mradi wa maji wa Mhangu – Ilogi awamu ya kwanza umekamilika na tayari unatoa huduma katika Kijiji cha Ilogi. Utekelezaji wa awamu ya pili unaendelea na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Desemba, 2022. Mradi huu ukikamilika utakuwa na bomba lenye urefu wa kilomita 37.5, matenki manne yenye jumla ya ujazo wa lita 440,000 na vituo 32 na kunufaisha wananchi wapatao 24,436.
MHE. CECIL D. MWAMBE K.n.y. MHE. KATANI A. KATANI aliuliza: -

Je, ni lini mradi wa maji wa Mkwiti utakamilika ili kupunguza tatizo la maji katika Kata ya Mangombya, Mkwiti na Litehu?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Katani Ahmed Katani Mbunge wa Tandahimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mradi wa maji wa Mkwiti utakaohudumia Kata za Mangombya, Mkwiti na Litehu zenye jumla ya vijiji 16. Mradi huu unatekelezwa kwa awamu nne ambapo awamu ya kwanza na ya pili zimekamilika na ilihusisha ujenzi wa bomba kuu lenye urefu wa kilometa 13 na ufungaji wa pampu kwenye chanzo. Utekelezaji wa awamu ya tatu na ya nne unaendelea na umefikia asilimia 50 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022. Kazi zinazofanyika ni pamoja na ujenzi wa matanki sita yenye jumla ya ujazo wa lita 300,000, ulazaji wa bomba lenye urefu wa kilomita 89 na ujenzi wa vioski 48 vya kuchotea maji. Ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, ni lini RUWASA Nyasa itapatiwa gari ili kurahisisha utendaji kazi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI k.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eng. Stella Martin Manyanya Mbunge wa Nyasa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuijengea uwezo RUWASA Mkoa wa Ruvuma ili iweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu. Katika mwaka wa fedha 2022/2023 jumla ya magari 86 yatanunuliwa na kupelekwa kwenye Wilaya mbalimbali nchini ikiwemo Wilaya ya Nyasa. Ahsante.
MHE. DANIEL T. AWACK aliuliza: -

Je, ni lini itatolewa bei elekezi ya maji katika Karatu ili kuondoa tofauti kati ya KARUWASA wanaouza unit 1 Sh.1,700 na KAVIWASU unit 1 Sh.3,000?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Tlemai Awack, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, dhamira ya Serikali ni kuhakikisha hakuna changamoto katika ulipaji wa bili za maji kwa wananchi. Hivyo, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023, imeviunganisha vyombo vya usimamizi wa huduma ya maji KARUWASA na KAVIWASU na kuunda chombo kimoja cha KARUWASA ambacho kitakuwa imara ili kiweze kutoa huduma ya maji kwa ufanisi katika eneo lote la Mji wa Karatu.

Mheshimiwa Spika, bei elekezi ya kuanzia kwa uniti moja ya maji imeshatolewa na inatumika. Aidha, marekebisho yataendelea kufanyika kwa kuzingatia miongozo kutoka EWURA.
MHE. KAVEJURU E. FELIX K.n.y. MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha Mradi wa Maji Kata ya Kazuramimba?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza Mradi wa Maji wa Kata ya Kazuramimba ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 90. Kazi zilizofanyika ni pamoja na ulazaji wa bomba kuu kilometa 3.3, ulazaji wa mabomba ya usambazaji Kilometa 26.7 na ujenzi wa tanki la ukubwa wa lita 470,000. Ujenzi wa mradi unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Novemba, 2022.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa Mradi wa Maji Mkinga kutoka Mto Zigi au Kinyatu utaanza kutekelezwa?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dunstani Luka Kitandula, Mbunge wa Jimbo la Mkinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuboresha huduma ya maji kwa wananchi wa Wilaya ya Mkinga pamoja na maeneo ya pembezoni, Serikali imekamilisha usanifu wa mradi wa maji wa Mkinga kwa kutumia chanzo cha maji cha Mto Zigi mwezi Machi, 2022. Aidha, taratibu za kupata mkandarasi zinaendelea na anatarajiwa kuanza kazi mwezi Juni, 2022 na utekelezaji utaendelea katika mwaka wa fedha 2022/2023.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga upya Bwawa la Kasamwa na kutenganisha mwingiliano wa binadamu na mifugo?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Bwawa la Kasamwa lilijengwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kutoa huduma za maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu, viwanda, kunyweshea mifugo pamoja na kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali itafanya usanifu kwa ajili ya kukarabati bwawa hilo ambapo pia itajumuisha miundombinu kwa ajili ya kunyweshea mifugo.
MHE. MARTHA F. MARIKI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakuja na mpango wa kutoa Maji Ziwa Tanganyika na kuyapeleka Mkoa wa Katavi?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Festo Mariki Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hali ya huduma ya upatikanaji wa maji Mkoa wa Katavi ni asilimia 71 kwa Vijijini na asilimia 60 kwa Mjini. Katika kuboresha huduma ya maji Serikali imeanza kutekeleza miradi ya maji kwa kutumia chanzo cha Ziwa Tanganyika. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 mradi unaoendelea kutekeleza ni Mradi wa Maji Karema katika Wilaya ya Tanganyika utakaohudumia vijiji vya Kapalamsenga na Songambele.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kutumia Maziwa Makuu kunufaisha wananchi waishio karibu na vyanzo hivyo ikiwemo wananchi wa Mkoa wa Katavi uliopo karibu na Ziwa Tanganyika.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali itaajiri Mtaalam Mshauri wa kufanya usanifu wa kina wa ujenzi wa miundombinu wa chanzo cha maji (intake) chenye uwezo wa kuzalisha maji mengi kutoka Ziwa Tanganyika na kuwezesha wananchi wa Wilaya za Tanganyika, Mlele, Mpanda na maeneo ya karibu kunufaika na chanzo hicho.
MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasambaza maji katika Wilaya ya Nkasi kutoka Ziwa Tanganyika?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kutumia Maziwa Makuu kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi waishio karibu na vyanzo hivyo ikiwemo wananchi wa Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa. Katika kutimiza azma hiyo, Serikali imeanza kutumia Ziwa Tanganyika kuwanufaisha wananchi wa Wilaya ya Nkasi ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imekamilisha miradi ya maji ya Kirando, Kamwanda, Mkinga na mradi wa maji Kabwe.

Kukamilika kwa miradi hiyo kumeboresha hali ya upatikanaji wa huduma maji Wilayani Nkasi kutoka asilimia 47 hadi asilimia 53.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali itaendelea na usanifu wa miradi ya maji kupitia chanzo cha Ziwa Tanganyika kwenye vijiji 10 vya Kilambo, Kala na Tundu Kata ya Kala, Izinga, Mwinza na Wampembe Kata ya Wampembe, Ninde, Kisambala na Namasi Kata ya Ninde na Mandakerenge Kata ya Kipili. Vilevile, katika mwaka 2022/2023, usanifu utafanyika kwa ajili ya kupeleka maji Mji wa Namanyere pamoja na vijiji vilivyoko kilomita 12 kila upande ambapo bomba kuu litapita. Usanifu huo unatarajiwa kukamilika katika robo ya pili ya mwaka wa fedha 2022/2023 na baadaye ujenzi utaendelea.
MHE. NDAISABA G. RUHORO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Mradi wa Maji Kabanga?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII K.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro Mbunge wa Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Mradi wa Maji Kabanga unaendelea kwa gharama ya Shilingi 941,351,342.74. Utekelezaji wa mradi huu umefikia asilimia 75 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2023 na kuhudumia wananchi zaidi ya 15,000 wa Vijiji vya Kabanga, Murukukumbo na Kumwuzuza. Kazi zilizofanyika ni pamoja na ujenzi wa dakio, nyumba ya mashine, tanki la kukusanyia maji lenye ujazo wa lita 120,000, tanki la kuhifadhia maji lenye ujazo wa lita 230,000 na ujenzi wa viosk vitatu. Kazi zinazoendelea ni pamoja na uchimbaji wa mitaro kwa ajili ya kulaza mabomba umbali wa kilometa 20.694 na ukamilishaji wa ofisi ya CBWSO.
MHE. IDDI K. IDDI K.n.y. MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga chujio la kuchuja na kutibu maji toka chanzo cha maji Nyamtukuza kabla ya kuyapeleka kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII K.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyangh’wale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali Serikali ilipanga kujenga chujio la maji kwenye chanzo cha maji cha Nyamtukuza kwa ajili ya kuwapatia huduma ya maji safi na salama wananchi wa vijiji vya Nyangh’wale. Hata hivyo, kwa kuwa bomba kuu la KASHWASA linapita karibu, Serikali ilifanya usanifu wa kuchukua maji eneo la Mhangu na kubaini unafuu wa gharama ikilinganishwa na ujenzi wa chujio hivyo ilijenga mradi kupitia bomba hilo na hadi sasa vijiji 21 vinanufaika. Maji ya KASHWASA tayari yametibiwa na ni safi na salama na yatatosheleza mahitaji ya maji kwa wananchi wa Nyangh’wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa chujio sasa zinatumika kujenga miundombinu ya kusambaza maji kwenye vijiji vya Nyaruguguna, Nyamgogwa, Iseni, Nyangalamila, Kabiga, Nwiga, Bukungu, Bumanda, Kanegere, Mimbili na Isonda. Serikali itajenga chujio la kuchuja na kutibu maji Nyamtukuza kulingana na mahitaji ya huko baadaye.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuvipatia maji Vijiji vilivyopo mwambao wa Ziwa Nyasa?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika; naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Ziwa Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwambao wa Ziwa Nyasa una vijiji 39 na kati ya hivyo vijiji 18 vinapata huduma ya maji na vijiji 21 havina. Katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali inatekeleza Miradi ya Maji ya Lituhi, Liuli, Ngumbo, Puulu, Songambele na Nangombo-Kilosa, inayotarajia kukamilika katika mwaka wa fedha 2023/2024 na kunufaisha vijiji 17.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, Serikali ipo katika hatua za mwisho kukamilisha usanifu wa Mradi wa Maji Ndengele-Mbuyula utakaohudumia vijiji vitatu na itaendelea na usanifu katika Kijiji cha Ndonga. Ujenzi wa miradi hii utafanyika katika mwaka wa fedha 2023/2024.
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE K.n.y. MHE. JUSTIN L. NYAMOGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa mradi wa maji wa Kihesa Mgagao, Masege hadi Masalali - Kilolo?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa mradi wa maji katika vijiji vya Kihesa Mgagao, Masege hadi Masalali upo kwenye hatua za mwisho za kumwajiri Mkandarasi. Utekelezaji wa mradi utaanza Mwezi Mei, 2023 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Mei, 2024. Kazi zitakazofanyika ni pamoja na ujenzi wa matenki matatu (3) yenye jumla ya ujazo wa lita 250,000, ujenzi wa mtandao wa mabomba ya maji yenye urefu wa kilometa 25.4 na ujenzi wa vituo 25 vya kuchotea maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa mradi huo kutanufaisha wananchi wapatao 9,006 waishio kwenye vijiji hivyo.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kupeleka maji ya Ziwa Victoria katika Kata za Ikunda, Mwakata, Menga, Shilela na Lunguya - Msalala?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekamilisha usanifu wa upanuzi wa miradi ya maji ya Mhangu - Ilogi na Nduku - Busangi itakayohudumia Kata za Ikunda, Mwakata, Menga, Shilela na Lunguya zilizopo Wilayani Msalala. Kwa sasa taratibu za kumpata Mkandarasi kwa ajili ya ujenzi zinaendelea na ujenzi utaanza katika mwaka wa fedha 2023/2024.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka maji katika Kata za Maruku, Karabagaine, Nyakato, Kunazi, Katoma, Kemondo na Bujugo Jirani na Bukoba Manispaa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekamilisha utekelezaji wa mradi wa maji Kata ya Katoma na wananchi wanapata huduma ya maji. Vilevile, utekelezaji wa miradi ya maji unaendelea kwenye Kata za karabagaine na Nyakato ambapo miradi imekamilika katika vijiji vya Itahwa, Kabale na Burugo. Maeneo ya Kemondo na Kunazi utekelezaji wa mradi unaendelea na umefikia asilimia 88. Kwa Kata za Maruku na Bujugo, Serikali ipo katika hatua za mwisho za kumuajiri Mkandarasi na ujenzi utaanza mwezi Juni, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi kwenye vijiji vilivyobaki katika Kata za Karabagaine na Nyakato.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -
Je, lini Serikali itaanza na kukamilisha ujenzi wa mradi wa maji toka Ziwa Victoria kwenda Biharamulo?

WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa Mji wa Biharamulo ni asilimia 86. Katika kupunguza kero ya maji kwa wakazi wa mji huo, Serikali ina mipango ya muda mfupi na mrefu. Katika mpango wa muda mfupi, Serikali inaendelea kutekeleza mradi wa kuboresha miundombinu ya maji Biharamulo, na kazi zinazotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa chujio, bomba kuu la urefu wa kilomita 2.8, tanki la ujazo wa lita milioni moja na ununuzi wa pampu yenye uwezo wa kusukuma maji lita laki 120 kwa saa. Utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 65 na unatarajia kukamilika mwezi Juni, 2023 na kuongeza huduma ya maji kufikia asilimia 90.

Mheshimiwa Spika, katika mpango wa muda mrefu, Serikali itajenga mradi mkubwa wa kutoa maji Ziwa Victoria kwenda Biharamulo. Usanifu wa mradi huo umekamilika na ujenzi unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2023/24.
MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza: -

Je, lini Serikali itatekeleza mradi wa kusambaza maji kutoka Mlandizi hadi Mzenga – Kisarawe?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Subira Khamis Mgalu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na usanifu wa kina wa mradi wa maji kutoka bomba kuu la DAWASA Mlandizi kupeleka kwenye vijiji 19 vya Wilaya ya Kisarawe vikiwemo vijiji vya Kata ya Mzenga. Usanifu huo unatarajia kukamilika mwezi Agosti, 2023 na ujenzi kufanyika katika mwaka wa fedha 2023/2024.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Kata za Mkalamo, Magamba Kwalukonge na Mkomazi Wilayani Korogwe?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua adha ya maji inayowakabili wananchi wa Kata za Mkalamo, Magamba, Kwalukonge na Mkomazi Wilayani Korogwe. Hatua mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa kukabiliana na hali hiyo na katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imechimba visima viwili virefu, kufunga pampu na kujenga tenki la lita 75,000 ambapo wananchi wa vijiji vya Magamba, Kwalukonge, Changalikwa na Makole Kata ya Magamba Kwalukonge wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa Kata zilizobaki, Serikali itajenga miradi ya maji kupitia chanzo cha Mto Pangani, Mtaalam ameajiriwa na anaanza kazi mwezi Mei, 2023 na utekelezaji wa miradi utafanyika katika mwaka wa fedha 2023/2024.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: -

Je, ni lini changamoto ya maji ndani ya Jimbo la Momba litatatuliwa?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe Mbunge wa Jimbo la Momba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua adha ya maji wanayopata Wananchi wa Wilaya ya Momba na tayari hatua zimeanza kuchukuliwa. Katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 miradi ya maji ya Msangano-Naming’ongo, Isanga - Kakozi na Tindingoma - Mlomba inaendelea kutekelezwa na itahudumia vijiji 11 vya Msangano, Nkala, Makamba, Naming'ongo, Yala, Ipata, Ntinga, Chindi, Isanga, Kakozi na Mlomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maji kupitia chanzo cha maji cha Mto Momba ili kuhakikisha wananchi katika vijiji vilivyobaki Wilayani Momba wanapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza.
MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza: -

Je, lini Serikali itakarabati miundombinu chakavu ya maji na kuhakikisha upatikanaji wa maji ya kutosha katika Mji wa Mbinga?
WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanza ukarabati wa miundombinu chakavu katika Mji wa Mbinga. Kazi zinazoendelea ni pamoja na ukarabati wa mabomba ya maji umbali wa kilometa 21, ukarabati wa kitekeo cha maji Ndengu na ununuzi wa dira za maji 2,500 kwa ajili ya kuunganisha wateja wapya. Utekelezaji wa kazi hizo unatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha wakazi wa Mji wa Mbinga wanapata huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza, Serikali imekamilisha usanifu wa Mradi wa Maji Mbinga utakaohusisha ujenzi wa vitekeo viwili vya maji, matenki matatu yenye jumla ya ujazo wa lita 450,000 na ulazaji wa mabomba umbali wa Kilometa 83. Utekelezaji wa mradi huo utafanyika katika mwaka wa fedha 2023/2024.