Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Rashid Ali Abdallah (6 total)

MHE. RASHID ALI ABDALLAH aliuliza:-

Kwa mujibu wa Sheria, Wizara ya Fedha inatoa Mikopo kwa wanafunzi wa Vyuo Vikuu nchini Tanzania.

Je, ni utaratibu gani mzuri wa kuondoa usumbufu kwa wanafunzi kupata mikopo yao kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ali Abdallah, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utoaji wa mikopo na ruzuku kwa wananafunzi wa elimu ya juu nchini unazingatia Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu Na. 9 ya mwaka 2004 kama ilivyorekebishwa, Kanuni za Utoaji Mikopo za mwaka 2008 na Mwongozo wa Utoaji Mikopo na Ruzuku kwa mwaka 2015/2016 ili kuweka vigezo, uwazi na urahisi katika utoaji wa mikopo.

Mheshimiwa Spika, fedha za mikopo zinalipwa kwa wanafunzi kupitia vyuo wanavyosoma ili kuhakikisha kuwa fedha zinawafikia walengwa kwa wakati. Tangu kuanza kwa utaratibu wa kuwalipa wanafunzi fedha za mikopo kupitia vyuoni, malalamiko yamepungua kwa takriban miaka minne sasa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwepo kwa mafanikio katika utekelezaji wa utaratibu huu, bado kuna changamoto katika ulipaji wa fedha hizo kwa wananfunzi kwa wakati kwa baadhi ya Vyuo Vikuu. Changamoto hizo husababishwa na ufinyu wa bajeti. Baadhi ya Vyuo Vikuu vyenye matawi kuwa na akaunti moja ya benki hali ambayo huchelewesha fedha kufika katika matawi; uongozi wa Chuo husika kutowapa wanafunzi taarifa ya kwenda kusaini kwa wakati ili walipwe mikopo yao; pamoja na baadhi ya wanafunzi kutosaini wakidhani wasiposaini hiyo mikopo hawatadaiwa watakapomaliza masomo yao.

Mheshimiwa Spika, ili kuondokana na changamoto hizi, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango, itaendelea kulipa kipaumbele suala la mikopo ya wanafunzi kwa Bodi ya Mikopo kupewa fedha kwa wakati. Serikali kupitia Bodi ya Mikopo, imeagiza Vyuo Vikuu vyote vyenye matawi kuhakikisha kuwa kila tawi linafungua akaunti ya benki ambayo fedha za wanafunzi wanaosoma katika matawi hayo zitaingizwa.
Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mikopo pia imetoa Waraka wa kuagiza vyuo vyote kuhakikisha wanafunzi wanalipwa ndani ya siku saba baada ya kupokea fedha kutoka Bodi ya Mikopo, kwani fedha hizo siyo za kuwekeza, bali ni kwa ajili ya wanafunzi.

Aidha, Wizara yangu imeiagiza Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu kufuatilia kwa karibu fedha zinazopelekwa Vyuoni zinawafikia wanafunzi wa kati. Sambamba na hilo, ili kuratibu upatikanaji wa taarifa za wanafunzi kwa wakati, kila Chuo kimeelekezwa kuwa na dawati maalum la Mikopo pamoja na Afisa Mikopo mwenye uwezo wa kushughulikia changamoto mbalimbali za mikopo ya wanafunzi katika chuo husika.

MHE. RASHID ALI ABDALLAH aliuliza:-
Ni jambo la kusikitisha sana kwa wananchi wanaosumbuliwa na saratani kuchelewa kupatiwa huduma katika Hospitali ya Ocean Road:-
Je, Serikali inalifahamu jambo hilo na inachukua hatua gani dhidi ya tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ali Abdallah, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inalitambua sana tatizo la upatikanaji huduma za matibabu katika taasisi ya Saratani ya Ocean Road na inafanya juhudi za ziada katika kuhakikisha changamoto hizi zinatatuliwa kwa kiasi kikubwa, kama siyo kwisha kabisa. Serikali pia hugharamia matibabu ya saratani kwa wananchi wake wanaobainika kuwa na ugonjwa huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mahitaji ya dawa za chemotherapy za kutibu saratani kwa mwaka 2015/2016 ilikuwa ni shilingi bilioni 7.2. Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Wizara imekuwa ikiongeza bajeti kwa ajili ya kununua dawa za saratani kupitia MSD na kuzisambaza kupitia hospitali husika, hususan Taasisi ya Saratani ya Ocean Road.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2011 Serikali kwa kushirikiana na Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa ya Bugando ilianza ujenzi wa Taasisi ya Saratani katika Hospitali hiyo. Taasisi hiyo itaongeza uwezo kukabiliana na ugonjwa wa saratani ambao hapo awali umekuwa ukitibiwa katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road pekee.
Mradi huo wa ujenzi wa jengo hilo lenye vyumba maalum sita (bunkers) kwa ajili ya kusimika vifaa, mitambo na mashine kubwa za mionzi (LINAC) umeshakamilika. Hatua inayofuata ni kusimika vifaa hivyo ambavyo tayari vimeshapokelewa hospitalini hapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mojawapo ya bunkers hizo ndiyo itaweka mashine hiyo ya LINAC ambayo ni mara ya kwanza kufungwa Tanzania.
Aidha, huduma za kutibu saratani kwa njia ya dawa za chemotherapy imeanza na hivyo wagonjwa wanaohitaji tiba ya aina hiyo hupewa.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH aliuliza:-
Nchi inakuwa na amani pale ambapo kuna ulinzi imara.
Je, ni utaratibu upi mzuri wa kuimarisha ulinzi Bungeni?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ali Abdallah, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina utaratibu za kulinda maeneo yote tete kwa ustawi wa jamiii husika ikiwa ni pamoja na Bunge letu Tukufu. Kuna ulinzi wa kutumia vifaa vya kisasa na vinginevyo ambavyo ni automated, ulinzi unaoonekana na ule usioonekana ambao hufanywa na askari na ule unaofanywa na wanyama kama mbwa. Yote haya hufanyika kwa pamoja na tunakuwa na ulinzi imara katika maeneo yetu kwani huwezi kutegemea aina moja tu ya ulinzi.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH aliuliza:-
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) mara nyingi hutumika kwa kutoa mikopo kwa Serikali kwa ajili ya maendeleo ya jamii.
Je, ni utaratibu gani wa kisheria unaofanyika ili kuhakikisha fedha za wanachama zinalindwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K. n. y. WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ali Abdallah, Mbunge wa Tumbe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ni mpango wa kisheria wa kuchangia huduma za matibabu ulioanzaishwa kutekeleza sera ya uchangiajia wa huduma za afya ya mwaka 1993 kupitia utaratibu wa wananchi kuchangia gharama za matibabu kabla ya kuugua.
Mheshimiwa Spika, ili kuufanya mfuko huu uwe endelevu, Mfuko huwekeza fedha za ziada katika vitega uchumi mbalimbali vya muda mfupi na mrefu vyenye lengo la kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa ujumla wake. Uwekezaji huu pia unajumuisha mikopo kwa Serikali kwa ajili ya maendeleo ya jamii. Uwekezaji unaofanywa na NHIF ni jukumu mojawapo la kisheria linalotekelezwa chini ya Sheria ya Mfuko wa Bima ya Afya ya mwaka 1999 ambao pia unasimamiwa na Sera ya Mfuko wa Bima ya Afya ya Uwekezaji pamoja na miongozo ya uwekezaji kama ilivyotolewa na Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii ikishirikiana na Benki Kuu ya Tanzania.
Mheshimiwa Spika, kazi mojawapo ya msingi ya mamlaka ya usimamizi wa sekta ya hifadhi ya jamii ikishirikiana na Benki Kuu ya Tanzania ni kutetea na kulinda maslahi ya wanachama kwa kuhakikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii inaelekeza uwekezaji wake katika vyanzo vya uwekezaji vilivyo salama na vyenye tija kwa wanachama na taifa kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa kupitia utaratibu huu nilioueleza, fedha za NHIF zipo salama. Aidha, kwa mujibu wa tathimini ya nne uhai wa Mfuko (actuarial valuation) iliyofanywa mwaka 2013 imeonesha uwezo wa mfuko kifedha na uendelevu wake ni hadi kufikia mwaka 2040.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH aliuliza:-
Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama vile LAPF, PSPF, PPF, NSSF na NHIF imesaidia sana kutoa mikopo hasa kwa Serikali kwa ajili ya maendeleo ya jamii:-
Je, Serikali imefanya juhudi gani kurejesha mikopo hiyo kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Ali Abdallah, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Serikali ilifanya uhakiki wa deni la Mifuko ya Hifadhi ya Jamii linalotokana na mikopo ya uwekezaji kwenye miradi mbalimbali ili kuandaa utaratibu wa malipo. Jumla ya deni lililowasilishwa Serikalini kwa ajili ya uhakiki kwa mifuko yote ni shilingi trilioni 2.1 na deni lililokubalika baada ya uhakiki ni shilingi trilioni 1.2.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya uhakiki kukamilika, Serikali ilianza kuandaa utaratibu wa kulipa deni hilo kwa kutumia hati fungani maalum zilizotarajiwa kuiva ndani ya kipindi cha kati ya miaka mitatu (3) na 20. Hata hivyo, wakati zoezi la kuandaa hati fungani likiendelea, Serikali ilipendekeza na Bunge lako Tukufu kuridhia mapendekezo ya Serikali ya kuunganisha Mifuko ya Pensheni na kuunda Mifuko miwili mmoja kwa ajili ya sekta ya umma na mwingine kwa ajili ya sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua hiyo, ilisababisha Serikali kusitisha zoezi la kuandaa na kutoa hati fungani maalum hadi hapo taratibu za kuunganisha Mifuko ya Pensheni zitakapokamilika.
MHE. RASHID ALI ABDALLAH aliuliza:-

Moja ya Dira ya Taifa kupitia Wizara ya Afya ni huduma bora ya afya ya wazazi na kupunguza vifo vya watoto na wazazi:-

Je, ni kwa kiasi gani Dira hii imetekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah, Mbunge wa Tumbe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto huandaa Sera na miongozo mbalimbali yakiwemo masuala ya afya ya uzazi na mtoto. Kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga ni suala linalopewa kipaumbele cha kwanza katika Wizara. Dhamira hii inaonekana na kuthibitishwa katika miongozo mbalimbli ya Serikali kama vile Sera ya Taifa ya Afya ya mwaka 2007; Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025; Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA); Mpango Mkakati wa Nne wa Afya; Mkakati wa Kupunguza na Kuimarisha Afya ya Uzazi, Watoto na Vijana; na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Wizara ni kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi kutoka 556 kwa kila vizazi hai 100,000 hadi 292 kwa kila vizazi hai 100,000 na kupunguza vifo vya watoto kutoka 21 kwa kila vizazi hai 1,000 hadi 16 kwa kila vizazi hai 1,000 ifikapo mwaka 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanikiwa kuongeza kiwango cha akina mama wanaojifungulia katika vituo vya kutolea huduma za afya kutoka asilimia 51 mwaka 2012 hadi asilimia 73 mwaka 2018. Aidha, wanawake wajawazito wanaohudumiwa na watoa huduma wenye ujuzi wameongezeka kutoka asilimia 40 mwaka 2012 hadi asilimia 72 mwaka 2018. Idadi ya wanawake wajawazito wanaohudhuria kliniki, mahudhurio manne na zaidi wameongezeka kutoka asilimia 46 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 57 mwaka 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti uliofanyika mwaka 2015/2016 unaonesha kwamba vifo vya watoto wenye umri chini ya miaka mitano, vimepungua kutoka 90 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2010 na kufikia 67 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2016. Vilevile, vifo vya kina mama vimepungua kutoka 578 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2010 na kufikia 556 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2016. Ni matarajio yetu kuwa utafiti unaofuata wa mwaka 2019/ 2020 utatupa matokeo chanya zaidi katika kupunguza vifo vya akinamama na wajawazito Tanzania.