Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. January Yusuf Makamba (32 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii. Naanza moja kwa moja kwa kutoa pongezi kwa hotuba nzuri aliyoitoa Rais wetu mpendwa, hotuba ambayo imetoa dira na mwelekeo wa Tanzania mpya. Kwa kauli ya hotuba ile na vitendo vilivyofuatia baada yake, tunaanza kuiona kabisa safari ya kupata Taifa jipya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, safari hii haitakuwa nyepesi, itakuwa ngumu, tutajaribiwa njiani, tutakejeliwa, tutakebehiwa, tutatiwa mashaka kuhusu mwenendo wetu, kuhusu mwelekeo wetu, lakini napenda kuwasihi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba tumuunge mkono Mheshimiwa Rais. Unapotaka kutengeneza keki ya mayai au chapati za mayai ni lazima upasue mayai. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, zamani kulikuwa na dawa zimeandikwa shake well before use, lazima utikise ndipo unywe dawa, ndipo ifanye kazi. Kwa hiyo, mitikisiko hii inayotokea ni sehemu ya kujenga Taifa jipya na wala watu wasipate mashaka wala wasiwasi kwamba nchi yetu inaelekea katika mwelekeo ambao sio wenyewe. Tulifika mahali tulihitaji Rais wa aina hii na tumempata na tumuunge mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumze kuhusu Zanzibar. Uchaguzi ni mchakato wa kikatiba na ni mchakato wa kisheria. Wakati tulipoamua kuingia kwenye Mfumo wa Vyama Vingi, tulibadilisha Katiba yetu, tukatengeneza taasisi zitakazotusaidia kuendesha uchaguzi wa ushindani na sheria ambazo zitatusaidia kuendesha siasa ya ushindani.
Kwa upande wa Zanzibar, Katiba ya Zanzibar Ibara ya 119 iliweka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ambayo ilipewa majukumu na mamlaka ya namna ya kufanya na ikapewa uhuru mkubwa. Vilevile ikatungwa Sheria Na. 11 ya mwaka 1984 na ikabadilishwa mara kadhaa ili kukidhi mahitaji ya siasa ya ushindani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar Kifungu cha 5(a) kinasema kwamba; “Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ina jukumu la usimamizi wa jumla wa mwenendo wa uchaguzi.” Maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba Tume imepewa nguvu na Mamlaka ya Kikatiba na Kisheria kufuta matokeo ya uchaguzi pale inapojiridhisha kwamba sababu na kasoro zilizojitokeza kwenye uchaguzi haziwezi kutoa matokeo yanayoakisi utashi wa watu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mamlaka ya Tume kuhusu kufuta uchaguzi wa Zanzibar hayana mashaka yoyote; hayana mashaka ndani ya Katiba, wala ndani ya sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ilitoa sababu nane za kufuta matokeo. Sababu mojawapo ikiwa ni malalamiko ya vyama vya siasa; ikiwa ni mgombea mmoja kujitangaza kwamba ameshinda ambapo ni kinyume kabisa na sheria, jambo ambalo lingeweza kupelekea machafuko na mtafaruku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ilikaa katika Mkutano wake wa tarehe 28 Oktoba, 2015 na kupitisha uamuzi wa kufuta matokeo yale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Katiba ya Zanzibar upo utaratibu wa Tume kufanya maamuzi. Ibara ya 119(10), kwamba Tume itakapokaa maamuzi yake ni halali anapokuwepo Mwenyekiti au Makamu na wajumbe wengine wanne. Vilevile Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar inatamka kwamba kanuni, maelezo na matangazo yote ambayo Tume ina mamlaka ya kutunga au kutoa, yatahesabika kwamba yametungwa kisheria kama yamewekwa sahihi na Mwenyekiti wa Tume au Mkurugenzi wa Uchaguzi. (Makofi)
Tangazo lililotolewa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar kufuta matokeo kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar ni tangazo halali kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile baada ya hapo tangazo lile, kama invyohitajika kwenye Katiba, liliwekwa kwenye Gazeti la Serikali kama hati ya kisheria namba 130 kwenye GN Namba 6587 ya tarehe 6 Novemba, 2015. Kwa hiyo, mjadala wa mamlaka ya Tume ya Uchaguzi kuhusu kufuta matokeo yale haupaswi kuwepo kwa sababu mamlaka yale inayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 21 Januari , 2016 Tume iliamua na kutangaza tarehe ya kurudiwa kwa uchaguzi. Kama Katiba inavyoelekeza katika Ibara ya 119 (10) kwamba maamuzi ya Tume ili yafanyike, ni lazima akidi itimie na lazima wengi wakubaliane na uamuzi ule.
Katika kikao cha Tume cha tarehe 21 mwezi wa Kwanza cha kuamua kutangaza kurudiwa kwa uchaguzi, akidi ilitimia na wengi walikubaliana na uamuzi ule. Kwa hiyo, uamuzi ule ni halali kisheria na Kikatiba. Katiba ya Zanzibar inasema kwamba hakuna mwenye mamlaka, hata Mahakama ya kuhoji au kuchunguza maamuzi yanayotolewa na Tume kuhusu uchaguzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wote tunajua kwamba uamuzi ule ulikuwa halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu lazima iendelee kuwa nchi ya amani, ni lazima iendelee kuwa nchi ya utulivu na msingi wa amani na utulivu ni kuheshimu Katiba na sheria ambazo tumezitunga sisi wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine linalozungumzwa ni kwamba kama matokeo ya uchaguzi ulioendeshwa na Tume Zanzibar yamekubalika na kwamba kama tuna Wabunge kutoka Zanzibar humu, iweje basi uchaguzi wa Zanzibar uharibike na matokeo yafutwe? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, chaguzi zile ni mbili tofauti, zimefanyika kwa Katiba mbili tofauti, Tume mbili tofauti, sheria mbili tofauti, madaftari mawili tofauti, utaratibu wa kuhesabu kura tofauti, wasimamizi tofauti, hata wino kuna wino wa NEC na wino wa ZEC. Kwa hiyo, haishangazi wala haistaajabishi kwamba uchaguzi mmoja ukaharibika mwingine ukawa halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachounganisha chaguzi hizi mbili ni kitu kimoja tu ni kwamba zilifanyika siku moja, lakini chaguzi hizi ni tofauti. Hoja kwamba kama uchaguzi huu ulikwenda sawa na mwingine siyo sawa, haina mashiko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwasihi wenzetu ambao wameamua kutafuta suluhu hii kwa nje ya Katiba na nje ya sheria, wanakosea na kwamba hakuna miongoni mwetu ambaye ana uwezo wala mamlaka ya kuiamrisha Tume ifanye kingine nje ya Katiba na nje ya sheria. Viongozi wa nchi yetu akiwemo Rais wetu, wamefanya jitihada kubwa na za kutosha kuhakikisha kwamba nchi yetu inaendele kuwa ya amani na kwamba maamuzi haya ya Tume ambayo hatuna mamlaka nayo, hayapelekei katika vurugu na mtafaruku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wajibu wa kulinda amani na umoja wa nchi yetu ni wajibu wa viongozi wa kisiasa. Maamuzi ambayo viongozi wa kisiasa wa Zanzibar watayachukua, kama yatakuwa ni maamuzi ya kusababisha vurugu na fujo na mtafaruku, basi damu ya Watanzania itakuwa mikononi mwao.
Sisi kwa upande wa Chama cha Mapinduzi na kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wajibu wetu ni kuhakikisha kwamba nchi yetu ianendelea kuwa ya amani, utulivu na usalama. Tunao wajibu wa kuheshimu maamuzi ya Tume na hicho ndicho tutakachofanya. Hatuna mamlaka ya kuiamrisha Tume ifanye vinginevyo kinyume na utaratibu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niliona niseme hayo. Yapo mengine yamezungumzwa yakiwemo masuala ya bomoa bomoa, tutayazungumza wakati wa michango ya kuchagia kwenye Mpango. Nashukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kushukuru sana wote waliochangia hoja hii, wamefika wachangiaji 43 waliochangia kwa maandishi na kwa kuzungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru sana kwa waliotuunga mkono, tunashukuru waliotuongezea mawazo na vilevile tunawashukuru waliotukosoa. Tutajibu baadhi ya hoja hapa kwa sababu muda ni mdogo na nyingine tutazijibu kwa maandishi na kuwakabidhi Waheshimiwa Wabunge kabla ya mwisho wa Mkutano huu wa Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa ambalo limezungumzwa kwa hisia kubwa na Wabunge wa pande zote linahusu uchaguzi wa Zanzibar na ndilo nitakaloanza nalo na nitaanza kwa kunukuu Katiba ya Zanzibar ambayo inatambulika na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 72(1) inasema; “Mahakama Kuu ya Zanzibar ndiyo pekee yenye mamlaka na uwezo wa kusikiliza na kuamua mashauri yote yanayohusiana na uchaguzi wa Zanzibar.” (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hayo ndiyo majibu yetu kuhusu uchaguzi wa Zanzibar, sitazungumza lolote hapa kwa sababu hapa siyo mahali pake, mahali pake pameelezwa kwenye Katiba ya Zanzibar. Vilio vyovyote vinavyohusu uchaguzi wa Zanzibar vikiletwa hapa Bungeni kwa kweli hapana msaada wowote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja iliyoko mbele yetu ni ya Muungano na Mazingira. Nianze tu kwa kusema kwamba mimi sikuzaliwa wakati wa Tanganyika, nimezaliwa wakati wa Tanzania kama ilivyo asilimia 92 ya Watanzania, sijui nchi yoyote zaidi ya Tanzania. Asilimia 92 ya Watanzania hawajui nchi yoyote zaidi ya Tanzania. Leo Tanzania hii uhalali wake ukihojiwa naumia binafsi.
Nadhani kwa viongozi ambao tumepewa dhamana na tuko kwenye Bunge ambalo juu lina nembo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni muhimu kabla hatujatoa maoni na kuzungumza kuhusu jambo kubwa kama hili tukajua shabaha yake, malengo yake, madhumuni yake na chimbuko la Muungano wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakumbuka kwamba kwenye miaka ya 1960 kulikuwa na hisia kubwa sana Barani Afrika za ukombozi, tulikuwa tunatafuta uhuru, tulikuwa tunataka kujikomboa na moja ya nyenzo kubwa za kujikomboa zilikuwa ni umoja wa watu wa Afrika. Hisia hizo za ukombozi zilihamasisha tuungane. Sisi bahati yetu Watanganyika na Wazanzibari Muungano wetu ulikuwa ni kurasimisha udugu ambao tayari upo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waasisi wa Muungano walikuwa na maarifa makubwa, walitafakari, walifikiria sana aina ya Muungano unaoendana na mazingira ya nchi yetu, aina ya Muungano unaoendana na ukubwa wa pande zote mbili, idadi ya pande zote mbili, tamaduni zetu na muingiliano ambao ulikuwa tayari umeshajitokeza kabla ya Muungano. Wale wazee walifikiria yote tunayoyazungumza sasa, Serikali hizi, zile na zile. Walipoamua, ndiyo maana Muungano huu umedumu, hawakuamua kwa pupa, hawakuamua kwa papara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama mwanafunzi wa umoja wa mwafrika, kama mwanafunzi wa historia ya Afrika, nimechukua muda mrefu kujifunza. Mmoja wa mwalimu wangu ambaye nimejifunza kwake yuko hapa, Balozi Job Lusinde. Nimetumia saa nyingi kuwa naye na moja ya swali nililomuuliza ni kwamba hebu niambie ilikuwaje, mliamuaje, chimbuko lake lilikuwa nini, nani alianzisha wazo! Nawasishi viongozi wenzangu Wabunge kwamba kama tunataka kuupa jina baya Muungano angalau tujue basi chimbuko lake. Naamini kwamba tukijua chimbuko lake, shabaha yake, malengo yake, kidogo tutapunguza ukali wa lugha tunayoitumia katika kuupa jina baya Muungano wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano wetu ulikuwa ni sehemu ndogo ya mradi mkubwa wa ukombozi wa mwafrika. Baadhi wanadhani kwamba umoja wetu sisi hauhitajiki sasa hivi, lakini leo unahitajika zaidi kuliko ilivyokuwa mwaka 1964. Kuna nchi nyingine zimeungana miaka 200 iliyopita, Marekani kwa mfano, zile federal government wana miaka zaidi ya 200 na hawajamaliza changamoto za muungano wao lakini hawazungumzii kuuvunja kwa sababu ya changamoto zilizopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliaswa na waasisi wa nchi yetu kwamba sisi ambao tunatafuta kuwa nchi zinazoendelea tunahitaji umoja zaidi kuliko wengine. Inawezekana baadhi yetu hatuoni mantiki, hatuoni busara waliyoiona waasisi wa Muungano wetu, hiyo ni sawa kabisa kwa sababu watu tunatofautiana. Wito wangu tu ni kwamba hebu tu-moderate lugha zetu kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma na nimesikiliza taarifa ya Kambi ya Upinzani kuhusu Muungano na mambo mengineyo na nimesikitishwa sana na baadhi ya lugha zilizotumika mle. Baadhi ya mambo yamejibiwa na Waziri Mheshimiwa Dkt. Mwinyi lakini kutumia maneno kwenye taarifa ile ya ukoloni na unyonyaji unaofanywa na Tanganyika dhidi ya Zanzibar, ni lugha ya kutugawa Watanzania. Inawezekana kuna mambo yanayoleta manung‟uniko kwenye Muungano, ni kweli inawezekana, lakini kwenda kwenye kiwango hiki cha kutumia maneno haya ya ukoloni na unyonyaji unaofanywa na Tanganyika dhidi ya Zanzibar ni lugha ambayo unapolaumiwa kwamba hupendi muungano huwezi kukataa kwa sababu umetumia lugha hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Jeshi la Tanganyika ameshajibu Mheshimiwa Mwinyi. Niendelee tu kwa kusema kwamba, ndugu yangu wa Konde pale rafiki yangu sana Mheshimiwa Khatib, anasema kwamba Muungano huu haufai kwa sababu tuko maskini, tuliungana ili tuwe matajiri. Mimi nataka kumuambia kwamba kwa sababu tuko maskini ndiyo tunauhitaji zaidi Muungano wetu huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napata shida kuelewa kitu kimoja kwamba Muungano haufai lakini Ubunge wa Bunge la Muungano unafaa. Mimi mantiki siioni labda ni ile ya kusema nyama ya nguruwe haramu, mchuzi wake halali. Inabidi tuamue kitu kimoja, kama hatuamini katika Muungano hatuwezi kuamini katika taasisi za Muungano ikiwemo Bunge la Muungano na hatuwezi kuwa sehemu ya taasisi za nchi ambayo hatuikubali na hatuiamini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja imetolewa kwenye Taarifa ya Upinzani kwamba ni CUF na napenda kunukuu hivyo hivyo, ni CUF na kiongozi wake Maalim Seif ndiyo pekee wanaolinda Muungano hadi kufikia ulipofikia, ukurasa wa 13, haya ni matusi kwa viongozi wote waliowahi kuongoza nchi hii. Kwa sababu wamefanya kazi kubwa ya kuulinda muungano, kuimarisha na kuujenga. CUF imeanza kuingia kwenye harakati mwaka 1992 wakati Muungano upo na unaendelea. Unaposema kwamba ni yeye peke yake tu ndiyo anafanya Muungano uwepo na udumu maana yake Mwalimu Nyerere, Karume, Mwinyi, Mkapa, Salmin Amour, Karume wa pili wote hawakuwa na maana yoyote isipokuwa kiongozi mmoja kule Zanzibar. Ndiyo maana nasema hebu tuya-moderate kidogo haya maneno ili angalau tutoke tukiwa tunaonekana tuna busara katika Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, baadhi ya mambo tutayajibu kwa maandishi kwa sababu hatuwezi kuyajibu yote hapa, niende kwenye michango ya baadhi ya Wabunge.
Mchango wa Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha kuhusu mapendekezo ya mgawanyo wa mapato jambo ambalo ni la msingi sana na jambo ambalo ndilo litapelekea kwenye ile dhana ya msingi ya kwamba kila upande uchangie na upate kulingana na mchango wake na ukubwa wake. Mheshimiwa Vuai amesema kwamba katika miaka kumi ya yeye kuwa Waziri Kiongozi na miaka mitatu ya kuwa Waziri kwenye Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hawakufanikiwa kulimaliza suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimueleze ndugu yangu kwamba Serikali hii imeingia madarakani miezi sita iliyopita, sisi hatutatumia miaka kumi kama aliyoitumia yeye katika Serikali iliyopita. Naomba niseme tu kwamba atupe nafasi na tumeanza, barua yangu ya kwanza kabisa kama Waziri katika Serikali hii na ilichelewa kwa sababu Waziri wa Fedha alichelewa kuteuliwa, ilikwenda kwa Waziri wa Fedha kuhusu kushirikiana kuandaa Waraka wa Baraza la Mawaziri wa kupitisha mapendekezo ya Tume ya Pamoja kuhusu mgawanyo wa mapato. Wizara ya Fedha imelifanyia kazi jambo hilo, Waraka upo tayari na wakati wowote utapelekwa kwenye Baraza la Mawaziri na kufanyiwa maamuzi ikiwemo uanzishwaji wa Akaunti ya Pamoja. Jambo hili litahusu pia mgawanyo wa zile asilimia 4.5 na kadhalika litafanyiwa kazi mara mapendekezo haya yatakapopitishwa kwa hiyo kazi inafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Menyekiti, lakini kabla ya hapo kuna arrangement za muda ambazo zinaendelea ikiwemo hiyo 4.5 kwa GBS na gawio la BOT. Pia VAT inayokusanywa Zanzibar kwa wafanyakazi wa Bara wanaofanya kazi Zanzibar inabaki Zanzibar na PAYE kwa maana hiyo na VAT inayokusanywa na TRA kwa upande wa Zanzibar inabaki Zanzibar na PAYE kwa wafanyakazi wa Bara wanaofanya kazi Zanzibar inabaki Zanzibar vilevile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Fakharia amezungumzia kuhusu Sekretarieti ya Ajira. Waziri wa Utumishi alitoa taarifa hapa kwamba tutafungua ofisi Zanzibar katika mwaka wa fedha unaokuja. Kwa hiyo, ofisi hiyo itafunguliwa na mimi niliwaunganisha Waziri wa Utumishi, dada yangu Mheshimiwa Angellah Kairuki na Waziri wa Utumishi, Mwalimu Haroun kule Zanzibar na Mheshimiwa Kairuki amepanga tarehe ya kwenda kutazama jengo na mahali ambapo ofisi itakuwepo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki nne zilizopita niliandika barua kwa Mawaziri kama saba hivi ambao wanasimamia taasisi za Muungano na kuwaomba kwamba watuletee mgawanyo wa ajira kati ya watumishi wa Zanzibar na watumishi wa Tanzania Bara kwenye taasisi za Muungano. Makubaliano yaliyokuwepo ni ya asilimia 79 kwa 21, makubaliano ya muda na Waheshimiwa Mawaziri hawa wameanza kunitumia. Nimeona kwa mfano Wizara ya Mambo ya Nje ambayo ndiyo inalalamikiwa sana kwa mwaka 2014/2015, katika nafasi 27 zilizotoka nafasi saba asilimia 26 zilikuwa Zanzibar na nafasi 20 asilimia 74 zilikuwa upande wa Tanzania Bara. Kwa hiyo, tumeanza na tutaendelea kwa sababu tunayo dhamira ya kuimarisha Muungano wetu, hatutachoka wala hatutachukizwa na maneneo ya kuudhi yanayozungumzwa dhidi ya muungano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko amezungumza na napenda nikiri kwamba tulipitiwa. Tulipitiwa kwa msingi kwamba sisi tulichukua human activities zote zinazoathiri mazingira ikiwemo wingi wa watu katika eneo dogo kwa wakati mmoja. Nakubali kwamba tungetaja wakimbizi kama ni changamoto mahsusi ya mazingira. Bahati nzuri maeneo aliyoyataja mimi nimefanya kazi miaka 20 iliyopita, nilikuwa Meneja wa Kambi ya Wakimbizi kule Mtabila, nafahamu Mtabila, Muyovosi, Lugufu, Nyarugusu, Kanembwa na kwingineko, kwa hiyo, Heru Juu, Heru Shingo na Mabanda kote ni kwetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nithibitishe kwamba kweli uharibu wa mazingira ni mkubwa sana unaotokana na uingiaji wa wakimbizi. Kwa hiyo, sisi kama Wizara tutawasiliana na Mashirika ya Kimataifa yanayohudumia wakimbizi kwamba kazi yao isiwe ni kulisha wakimbizi tu bali kutoa mchango kwenye kurudisha mazingira ya eneo lile kwenye hali nzuri. Mimi naahidi kutembelea mwenyewe kujionea mambo yalivyo huku. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, badhi ya Wabunge wamezungumzia masuala ya NEMC. Kwenye hotuba yetu tumezungumza jinsi ambavyo tutabadilisha na kupitia mfumo mzima wa kupitia vyeti vya tathmini ya athari kwa mazingira ili visiwe vinatumika kuchelewesha miradi ya uwekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Wabunge wamesema kwamba ofisi yetu ina bajeti ndogo na ina uwezo mdogo wa kitaasisi wa kudhibiti changamoto kubwa za mazingira. Mkitazama kwenye hotuba yetu ya bajeti katika maelezo ya Mfuko wa Mazingira, moja ya maelezo ya kazi ni kujenga uwezo wa kitaasisi wa Serikali ikiwemo NEMC kukabiliana na athari za mazingira. Kwa hiyo, Mfuko ule utakapoanza ofisi yetu itakuwa na uwezo mkubwa wa kifedha na rasilimali watu wa kuweza kudhibiti mazingira ikiwemo kuajiri Maafisa Wakaguzi wa Mazingira nchi nzima ili kila Halmashauri iwe na watumishi na hizi kamati kwenye kila kata na kijiji ili ziweze kufanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma Taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani ya dada yangu Mheshimiwa Pauline na napenda kumshuru sana kwamba kwa dhana na falsafa tunakubaliana bila shaka yoyote. Tunakubaliana kwamba mazingira ni jambo kubwa na pana na kule tunapoenda kwenye uchumi wa viwanda lazima tuzingatie hifadhi ya mazingira. Hilo tunakubaliana na tunashukuru kwa sehemu kubwa ushauri mlioutoa tutauzingatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mambo machache tu kwenye taarifa ile ambayo yanahitaji kurekebishwa. Kwenye ukurasa wa 19 ripoti imesema kwamba kwenye mradi wa DART tathmini ya mazingira haikufanyika. Nilitaka tu nisahihishe kwamba tathmini ilifanyika na cheti Na. EC/EIS/146 cha tarehe 30/6/2009 kilitolewa na masharti yalitolewa kwa waendesha mradi ule wa mambo ya kuzingatia katika hifadhi ya mazingira kwenye mkondo ule. Kwa hiyo, nilitaka niseme hilo la uelewa kwamba kwenye mradi ule tathmini ilifanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ripoti ya Mheshimiwa Pauline ilizungumzia kuhusu ripoti ya CAG ambayo ilitambua udhaifu kwenye utayari wa NEMC kwenye tasnia hii ya gesi na mafuta. Tumepokea sisi taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu na tutafanyia kazi mapendekezo yale. Mapendekezo yale utekelezaji wake unahitaji uwezo mkubwa na hakuna shaka yoyote kwamba tunaujenga. Niseme tu kwamba Sheria ya Gesi na Mafuta ambayo ndiyo ingetupa nguvu na uhalali sisi wana mazingira kuhusu ufuatiliaji imepitishwa mwaka jana tu na bahati nzuri sheria ile inatambua Sheria ya Mazingira na inatoa nafasi kwa NEMC kufanya kazi hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani imezungumzia miradi yenye shaka, miradi ambayo anasema inanukanuka ufisadi kidogo.
Mimi niseme tu kwamba tumepokea angalizo na mtu yeyote ambaye ananyoosha kidole kwamba mahali fulani inawezekana pana harufu anakusaidia. Sisi tunachukua taarifa hizo kama msaada kwa sababu Serikali hii imeamua kupambana na maovu ikiwemo rushwa na ufisadi. Kwa hiyo, haiwezekani nikasimama hapa nikakulaumu kwamba kwa nini umesema, nasimama hapa kukushukuru kwamba ni jambo ambalo tutalifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ila niseme tu kwamba miradi ile ina fedha za ndani kwa maana ya fedha zetu na za wafadhili, fedha za ndani zinaitwa counterpart fund. Kwa hiyo, siyo ajabu ukitazama makaratasi yetu ukakuta mradi wa ukuta, ukatazama karatasi la mfadhili ukakuta mradi wa ukuta kwa sababu fedha hizi zinakaa pamoja. Vilevile miradi hii inakaguliwa na CAG na katika miaka miwili iliyopita imepata hati safi lakini angalizo tumelipokea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu jana wakati nakutana na wataalam Wizarani nilielekeza kwamba wasiondoke kesho ili tupitie miradi yote. Kwa sababu kuna miradi mingi vya mazingira ambayo wakati mwingine hatuna taarifa za kina ili tuijue kila mradi ni upi, gharama zake ni zipi, umefikia wapi, unanufaisha watu wangapi, uliamuliwaje upelekwe huko ulikopelekwa na tunaweza kufanya maamuzi ya kuhakikisha kwamba miradi hii inawanufaisha watu wengi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea mchango wa Mheshimiwa Rehani Mwinyi anazungumzia kuhusu Mfuko wa Mazingira kwamba ndiyo mkombozi wa mazingira yetu na mimi nakubaliana naye asilimia 100. Katika mwaka huu wa fedha tunafanya mazungumzo ndani ya Serikali kuhusu vyanzo mbalimbali vya Mfuko huu na tunategemea support ya Bunge tutakapokuwa tumemaliza Serikalini. Mfuko huu kama tulivyosema kwenye hotuba yetu tunataka kwa kuanzia uwe na shilingi bilioni 100 lakini fedha hizi hazitoshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama ya kuhifadhi mazingira na kukabiliana na athari za mazingira na kurudisha mazingira katika hali yake ya kawaida kwa mwaka ni karibu shilingi bilioni 350. Ili turudi katika hali ambayo tunataka tuwe lazima fedha hizi zipatikane kwa miaka 17 mfululizo lakini sisi tunaomba shilingi bilioni 100. Nina imani kwamba ndani ya Serikali tutakubaliana kuhusu maeneo gani tunaweza kupata vyanzo hivyo ili Mfuko huu uanze ili tuwe na uwezo wa kuja katika maeneo yote kama aliyosema dada yangu Mheshimiwa Maufi kule Rukwa na kusaidia kurekebisha mazingira yaliyoharibika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatupaswi kutegemea wahisani kwa kuhifadhi mazingira ya nchi yetu kwa sababu huo ndiyo umekuwa mwelekeo mkubwa. Kuna dhana kwamba kwenye mazingira kuna hela nyingi za misaada lakini nchi hii ni ya kwetu, itarithiwa na watoto na wajukuu wetu, wahisani hapa siyo kwao. Kwa hiyo, sisi tuna wajibu mkubwa zaidi wa kuchanga ili kuhifadhi nchi yetu iendelee kuwepo siku nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tena kwa kushukuru kwa kupata fursa hii, nawashukuru Wabunge wote waliochangia, nashukuru kwamba mmetusaidia na naomba muendelee kutuunga mkono.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru wageni wetu walikokuja hapa siku ya leo ambao nimewataja, wale vijana wa mwaka 1964 waliochanganya udongo, Mzee Job Lusinde, wamekaa mpaka jioni hii na nina hakika matumbo yalikuwa yanawazunguka wakati Muungano ambao waliushuhudia unaundwa ulikuwa unadhalilishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie kwamba Serikali yao ipo imara katika kuulinda na kuhakikisha unaimarika ili kazi waliyoifanya iwe na matunda na iendelee kuwa sehemu ya urithi wa nchi yetu. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshmiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Napenda kumpongeza sana Dkt. Mpango, Naibu wake na Makatibu Wakuu na timu nzima ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa kazi nzuri ya kuandaa Mpango na kuuwasilisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumefarijika na kama Serikali tumeweka hifadhi ya mazingira kama vipaumbele muhimu katika mipango ya maendeleo ya nchi. Wakati wa bajeti Serikali italeta mipango ya kina ya kueleza tafsiri yake hasa ni nini na nini kitafanyika katika kuhakikisha kwamba hifadhi ya mazingira inazingatiwa katika mipango ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba nimefadhaika kidogo kwa michango iliyotoka hapa Bungeni kwa Wabunge walio wengi. Sisi Wabunge bila kujali Majimbo yetu, shida za watu wetu zinafanana bila kujali Jimbo ni la Upinzani au ni la CCM. Unapoikejeli Serikali, unapomkejeli Rais, unapowakejeli Mawaziri, angalau acha fursa ya uwezekano wa kuomba ushirikiano, kufanya kazi na Serikali hiyo hiyo, Rais na Mawaziri hao hao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ndiyo wenye Serikali, ndiyo tunapanga bajeti, ndiyo tunatekeleza maendeleo. Acha fursa ya ubinadamu wa kuweza kufanya kazi kwa pamoja. Mimi naelewa kwamba Upinzani kazi yao kulaumu, lakini ipo fursa ya kutoa Mpango mbadala. Hivi ninyi kwa kazi anayoifanya Mheshimiwa Magufuli leo, kipi mngefanya tofauti? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Bunge lililopita walikuwa wanatulaumu kuna uzembe, kuna ubadhirifu, kuna ufisadi; Mheshimiwa Magufuli anatibu uzembe, ubadhirifu, ufisadi bado mnatulaumu. What would you have done differently, leo kama mngekuwa na Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tishio hapa, watu wanazungumza amani itavurugika. Maarifa yaliyounda nchi yetu, maarifa yaliyounda Muungano wetu, maarifa yaliyolinda amani yetu mpaka leo ni makubwa kuliko ukomo wa kufikiri wa baadhi ya watu hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano wetu utadumu, amani yetu itadumu, nchi yetu itakuwa moja, hizi kauli za kutisha kwamba nchi italipuka, kutakuwa na mvurugano, tusiwatishe wananchi dola ipo na busara ya viongozi ambao walishiriki kwenye kuiunda nchi hii ipo. Wapo ndani ya Chama cha Mapinduzi, wapo ndani ya Serikali, nchi yetu itaendelea kuwa ya amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi wa suala la Zanzibar, naelewa haja ya kuonesha hisia ndani ya Bunge hili, lakini ufumbuzi haupo ndani ya Bunge hili. Ufumbuzi wa suala la Zanzibar haupo kwenye Ofisi za Mabalozi wa kigeni, ufumbuzi wa suala la Zanzibar haupo barabarani na mitaani. Ufumbuzi upo ndani ya Katiba na ndani ya Sheria za Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwamba tupo kama Serikali, tupo imara, tutafanya kazi yetu bila uoga, bila wasiwasi na Mheshimiwa Rais anafanya kazi nzuri, anaungwa mkono na Watanzania wote na wenzetu msione aibu kumuunga mkono. Siyo dhambi kama mtu anafanya kazi nzuri, kama Serikali inafanya kazi nzuri, kama Mawaziri wanafanya kazi nzuri, siyo dhambi kuwaunga mkono kwa sababu nchi yetu ni moja, kazi yetu ya kuleta maendeleo ni moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kuzipongeza Kamati zote mbili kwa kazi nzuri walizofanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niongezee kwenye maelezo ya Naibu Waziri wa Afya kuhusu suala la viroba na vifungashio vya plastiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili liko chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais na kanuni tuliandika kwa sababu linapigwa marufuku kwa kanuni za chini ya Sheria ya Mazingira. Suala hili ni mtambuka, lina upande wa kodi, kwa maana ya Wizara ya Fedha, lina upande wa viwanda, Wizara ya Viwanda na Biashara, lina upande wa Wizara ya Afya kwa maana ya TFDA na Udhibiti wa Vyakula na Vinywaji, lakini pia upande wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachofanya sasa ni Wizara zote kuandika karatasi ya pamoja ambayo itawezesha hatua tutakazochukua ziweze kutekelezwa kwa msukumo na mtazamo wa pamoja na kutapatikana balance kati ya haja ya kuhakikisha kwamba mapato yanaendelea kupatikana kwa nchi, lakini tunalinda afya za watu wetu na mazingira ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala hili linataka tafakuri ya kina ya pamoja ndani ya Serikali na ndiyo kinachofanyika na taarifa rasmi ya mwisho ya maamuzi hayo italetwa ndani ya Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na nakupongeza kwa namna ambavyo umetuongoza tangu asubuhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kutoa shukrani kwa wote waliochangia katika hoja yetu, kwanza kwa Kamati zote mbili, lakini pia kwa wasemaji wote wawili wa Kambi ya Upinzani kwenye masuala ya Muungano na Mazingira. Tumepokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge wote, kwa heshima na taadhima na moyo mkunjufu na ushauri mlioutoa tutaushughulikia. Wamechangia Wabunge 57 na kwa kweli kwa hoja ya siku moja kwa Wabunge 57 ni wengi, inaonyesha ni jinsi gani ambavyo kuna hamasa kubwa katika mambo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya mambo ambayo tutayatolea majibu sasa na kuna mengine tutayatolea majibu kwa maandishi na kuwapelekea Waheshimiwa Wabunge kwa sababu muda tulionao hapa hautatutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimefurahi na kufarijika kwamba yanapokuja masuala ya mazingira Waheshimiwa Wabunge wote wa upande huu na upande ule tunaungana. Kwa hiyo, napata faraja kwamba katika vitu vinavyoliungasha Bunge ni hifadhi ya mazingira. Hiyo inafanya kazi yangu iwe rahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninao marafiki wengi kwa upande ule kwa sababu ya masuala ya mazingira. Wapo watu ambao wanaonekana ni wakorofi kwa upande mmoja, lakini ukiingia ndani ya nyoyo zao ni wanamazingira wazuri sana hata Mheshimiwa Halima Mdee ni mwanamazingira mzuri sana, kwa hiyo, nawashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yangu ni kwamba kwa kadri siku zinavyoenda kila Mbunge atakuwa mwanamazingira na hili linatupa faraja kubwa sana. Hii inatokana na hali halisi ambayo Waheshimiwa Wabunge wanaiona katika majimbo yao na huko wanakoishi kuhusu uharibifu wa mazingira. Imani yangu ni kwamba hamasa hii itapelekea uwekezaji mkubwa katika hifadhi ya mazingira nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka kwenye hoja zilizotolewa. Kwanza, ni Mfuko wa Mazingira. Watu wengi wamezungumza kuhusu hili na nimesikitika kidogo dada yangu Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware ametulaumu kwamba miaka yote mfuko upo haujaanza, nilidhani kwamba angesema hongereni angalau kwa kuanza mwaka huu na ningependa utupe moyo na utuunge mkono kwa sababu ndio tumeanza na tunahitaji support yako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea namna ya kuupatia mfuko fedha. Sheria iliyoanzisha mfuko huu iko wazi kabisa vyanzo vimeainishwa humu. Katika nchi yetu zipo shughuli za kiuchumi na kiuzalishaji mali ambazo zinapelekea uharibifu wa mazingira. Kwa mfano, biashara ya mkaa ambapo Serikali inapata mapato, lakini biashara ile inaharibu mazingira; biashara ya magogo, Serikali inapata mapato lakini biashara ile inaharibu mazingira; uingizaji wa magari chakavu, Serikali ina-charge zaidi kwa shughuli hiyo lakini fedha hii haiji kwenye mazingira na uchimbaji wa madini vilevile kwenye leseni kuna fees zinatolewa. Kwa hiyo, sisi tunaongea na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuona ni namna gani katika hizi shughuli ambazo zinaharibu mazingira lakini Serikali inapata tozo basi sehemu ya tozo ije kwenye Mfuko wa Mazingira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Sheria ya Mazingira katika kifungu cha 213 kinaelezea sources of funds kwa mazingira na kinasema; “(a) such sums of money as may be appropriated by Parliament.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu hizi kinawapa nguvu Waheshimiwa Wabunge kuujaza mfuko huu pesa. Kwa hiyo, hatuna sababu ya kulalamika kuhusu fedha kidogo kwenye hifadhi ya mazingira wakati sisi wenyewe Wabunge tuna uwezo wa kuwa-appropriate pesa kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa hapa kuhusu suala la Baraza la Rufani. Na mimi nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge aliyesema kwamba Waziri siyo kazi yako kupiga faini, ile ni kazi ya Mkaguzi wa Mazingira na imeandikwa kwenye sheria. Nakubaliana kabisa na yaliyoelezwa kwamba wewe ni mamlaka ya rufaa kwa anayepigwa faini na hata mimi nikifanya kitendo kile naweza kukatiwa rufaa kwenye Baraza la Rufaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini moja ya changamoto ya kutokuwepo kwa Baraza ni mfuko huu kutokuwa na pesa kwa sababu ukienda kwenye sheria kifungu cha 205 vyanzo vya fedha za Baraza la Rufani kinasema ni Mfuko wa Mazingira. Kwa hiyo, kama Mfuko wa Mazingira hauna fedha Baraza la Rufani halipo. Kwa hiyo, utaona kuna muunganiko wa ujenzi wa kitaasisi wa hifadhi na usimamizi wa mazingira. Kwa hiyo, tukilimaliza suala la Mfuko wa Mazingira tutakuwa tumemaliza suala la Baraza la Rufani vilevile. Nadhani Mheshimiwa Gekul ndiye aliyezungumzia jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla kuhusu fedha kidogo kwenye hifadhi ya mazingira ukweli upo wazi, wote mnaona. Jawabu ni moja kupanga fedha zaidi na pili kuujaza mfuko. Hata hivyo, kuna jambo lingine tumelifanya na nimesema kwenye hotuba kwamba mwaka huu sasa tumefanikiwa kila Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Sekretarieti ya Mkoa na Wizara itakuwa na kifungu kwenye bajeti kinaitwa kifungu cha hifadhi ya mazingira kwa sasa hakuna. Wenzetu watakapokuwa na vifungu hivyo wataamka na kupanga shughuli za hifadhi za mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunahangaika kutafuta ufadhili kwenye hifadhi ya mazingira kutoka kwa wenzetu sehemu mbalimbali. Tumeeleza asubuhi kwamba kwa jitihada za ofisi yetu tumeweza kufanikisha upatikanaji wa shilingi bilioni 230 kwa ajili na mradi wa maji. Tunaendelea na nataka niwahakikishie kama Mungu akipenda na kama tutaendelea kuwepo kwenye nafasi hizi nikisimama tena hapa mwakani, nitakuja na habari nzuri zaidi kuhusu upatikanaji wa fedha nyingi zaidi kutokana na ufadhili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viroba Mwanasheria Mkuu ameliongelea sina haja ya kurudia sana lakini napenda kukumbusha tu kwamba Serikali ilitoa taarifa ya kwanza kabisa ya dhamira yake ya kupiga marufuku viroba na mifuko ya plastiki Bungeni hapa kwenye bajeti ya mwaka jana mwezi Mei na mpaka shughuli ile imesimamishwa ilikuwa Machi 1 ni miezi kumi. (Makofi)
Kwa hiyo, sikubaliani kabisa na hoja kwamba hakukuwa na taarifa ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichokuwepo ni kwamba wenzetu kwa kuzoea ile habari kwamba Serikali ikisema haitendi kuna watu kabisa waliingiza mitambo wakatengeneza stock mpya. Ukienda kwenye Hansard hapa Bungeni utaona hilo, lakini tarehe 16 Agosti, pia tukatoa taarifa kwa umma kwamba tutapiga marufuku viroba tarehe 01 Januari 2017, lakini unakutana na mtu anakuambia mimi nimeingiza mzigo juzi. Sasa kama unaagiza mzigo wakati ukiwa na taarifa kwamba Serikali ina dhamira gani kuhusu biashara hiyo yanayokukuta ni kwamba umeamua wewe mweyewe yakukute. Licha ya hivyo, Serikali itaendelea kufanya mazungumzo na wafanyabiashara hawa ili kuangalia utaratibu nzuri wa namna ya kumaliza kabisa shughuli hii. Wote tunakubaliana kuna manufaa makubwa zaidi kwenye kupiga marufuku shughuli hii kuliko kuacha iendelee, hilo halina ubishi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upandaji miti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kuhusu utaratibu wa upandaji miti hapa nchini. Tunafahamu kwamba tangu uhuru nchi yetu imefanya jitihada mbalimbali za kupanda miti, lakini hatukupa mafanikio ya kuridhisha. Mkakati mpya tulioutengeneza umezingatia sababu za kufeli kwa mipango ya siku za nyuma, umeshirikisha sekta binafsi na mamlaka zote, tumeandika kila kata hapa nchini inastawi mti gani na unapaswa kupandwa wakati gani. Mkakati huo tutautoa kwa ajili ya kuelimisha Wabunge na wananchi jinsi ya kuutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa nchini idadi ya miti yote iliyopo asilimia kumi tu ndiyo ya kupanda asilimia 90 ndio miti ya asili inayoota yenyewe. Kwa hiyo, namna nzuri ya kuwa na miti hapa nchini ni kuhifadhi ile ambayo tunayo tayari, ile miti ya asili. Kwa sehemu kubwa nchi yetu ina miti ya miyombo ambayo inaamka kwa haraka zaidi pale inapoachwa ikue. Kwa hiyo, kikubwa zaidi ni kuacha kupanda miti na kupanda miti vilevile lakini matumaini makubwa yapo kwenye kuhifadhi miti na misitu tuliyo nayo. Ipo miradi mingi zaidi na taratibu nyingi tutazitumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dada yangu Mheshimiwa Pauline amesema asubuhi kwamba kuna harufu ya kifisadi kwenye baadhi ya miradi, lakini hakutusaidia kwamba ni katika eneo gani hasa kwa sababu ufisadi upo wa namna nyingi. Je, ni kwenye procurement au malipo? Namwomba hata kwa kuninong’oneza anieleze ili nilishughulikie jambo hili kwa sababu ni jambo hatutaki liwepo kwenye ofisi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwakikishie kwamba miradi hii kwa masharti ya ufadhili wake kila mwaka inakaguliwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali. Kumefanyika ukaguzi 2013/2014, 2014/2015 na ripoti ya 2016 inakuja na wamejiridhisha kabisa kwamba miradi ile iko safi kabisa na inatekelezwa kwa kiwango kilichotarajiwa. Kwa hiyo, sisi tunaamini kabisa kwamba hakuna tatizo lolote lakini kama dada yangu Mheshimiwa Pauline una taarifa naomba unijulishe ili nianze kufuatilia hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu matumizi ya mkaa. Matumizi ya mkaa ni changamoto kubwa na ni sababu kubwa inayopelekea uharibifu wa mazingira nchini mwetu. Sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais tumeamua kuchukua leadership kwenye jambo hili kwa sababu ndugu yangu na mzee wangu Mheshimiwa Profesa Maghembe mkaa kwake ni chanzo cha mapato, wakati mimi kwangu mkaa ni uharibifu wa mazingira. Mimi nina interest kubwa zaidi nchi yetu ika- transition kutoka kwenye matumizi ya mkaa kwa sababu kwa kadri siku zinavyoenda nishati za kupikia mbadala zinaendelea kuwa nafuu na zinaweza kushindana kwenye soko la mkaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tulifanya kongamano kubwa ambalo tuliliongoza na wadau wote wa utengezaji wa mkaa. Tumeamua kuanzisha shindano kubwa kabisa la kitaifa na wale majasiriamali wote wanaoweza kutengeneza nishati mbadala waje watuonyeshe tutawapa zawadi. Zawadi ya kwanza kabisa itakuwa zaidi ya shilingi milioni 400 na tutawawezesha kupanua biashara yao hiyo, viwanda vya mkaa vitaanzishwa ili taratibu tuondoe mkaa kwenye soko siyo kwa kuupiga marufuku bali kwa kuufanya ushindwe kwa bei na nishati nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba kuna Wakuu wa Wilaya na baadhi ya maeneo wamepiga marufuku usafirishaji wa mkaa kutoka kwenye maeneo yao ni hatua njema. Hata hivyo, lazima twende nayo taratibu kwa sababu mji kama Dar es Salaam ambapo asilimia 60 ya mkaa unatumika Dar es Salaam na pale hakuna sehemu unaweza kuzalisha mkaa, kwa hiyo, lazima tuwezeshe watu kupata nishati inayolingana na bei ya mkaa ndipo tuweze kupinga marufuku kabisa matumizi ya mkaa. Huko ndiko tunakoelekea, hii road map ambayo tunakuja nayo itaeleza miaka mingapi na kwa utaratibu gani tutaondoa matumizi ya mkaa hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu pia katika mkaa unaozalishwa nchini kwa sehemu kubwa mkaa huo unakwenda kuchoma nyama Uarabuni. Ukienda kwenye bandari zile za Bagamoyo, Mbweni majahazi na majahazi yamejaa mkaa unaenda Unguja. Unguja haiwezi kutumia mkaa wote ule unaoenda kule, ukifika Unguja unapanda tena unaenda Mombasa - Shimoni. Ukifika kule unawekwa kwenye magunia mazuri made in Kenya unaenda kuchoma nyama Uarabuni. Nataka niombe ruhusa ya Mheshimiwa Rais niende Kenya nikazungumze na wenzetu ili tuweze kuona namna gani tunaweza kushirikiana pamoja na Wizara Maliasili kupiga kabisa marufuku suala hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea kuhusu namna tunavyoweza kuzibalisha taka ngumu ziwe rasilimali. Sisi kwenye ofisi yetu hazipiti wiki mbili tunapokea mwekezaji, mapendekezo, proposal ya mtu anayetaka kuzalisha umeme kwa kutumia taka. Bahati mbaya sana hawa watu wanaoleta hii miradi wanazunguka sana hawajui pa kuanzia. Wengine wanaanzia TANESCO, wengine Wizara ya Nishati, wengine TAMISEMI, wengine wanakuja kwetu na wengine wanakwenda EWURA. Kwa hiyo, matokeo yake ni kwamba hapa nchini mpaka sasa hakuna mradi uliofanikiwa kwa sababu hakuna mwongozo
na utaratibu wa kushughulikia miradi hii wakati taka zipo nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Makamu wa Rais mwezi Mei ataitisha kikao ambacho kitakuwa ni kati ya sisi Wizara ya Nishati, TAMISEMI Halmashauri za Majjiji zote EWURA na TANESCO na kikao hicho ndicho kitaamua kuhusu mwongozo wa kukaribisha uwekezaji wa sekta binafsi kwenye shughuli ya kuchakata kata. Kwa wale Waheshimiwa Wabunge ambao wamekuwa na hoja hizi, naomba wawe na subira Serikali itatoa mwongozo kutoka kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais kuhusu namna gani tunaweza kurahisisha na kuharakisha uwekezaji wa sekta binafsi katika kuchakata taka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mazingira ya bahari na pwani, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza kuhusu mambo mawili. Kwanza, uvuvi haramu lakini pili watu wanaokaa pwani wanajua jinsi fukwe zinazovyoliwa kutokana na mabadiliko ya tabianchi. Sisi ofisi yetu inao mkakati, Mheshimiwa Ghasia na Waheshimiwa wengine wameongea, mtakumbuka miezi mitatu iliyopita ofisi yetu sisi na mimi niliongoza nilikuwa Mwenyekiti wa kikao cha Mawaziri kama sita hivi tena wazito, Mheshimiwa Mwinyi, Mheshimiwa Mwingulu, Wizara ya TAMISEMI na Maliasili ambapo tulikaa na kutengeneza mkakati wa pamoja wa kukabiliana na uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wiki chache zijazo mtaona operesheni kubwa ya Kiserikali, tusingependa kuizungumza kwa sababu tunakabiliana na watu wanaofanya kazi shughuli haramu ambayo itamaliza kabisa tatizo hili la uvuvi haramu. Vilevile tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya mabadiliko ya tabia nchi katika maeneo ya kanda za Pwani kwa kujenga kuta kama tunavyojenga pale Ocean Road, Pangani, Kigamboni na Zanzibar lakini kupanda mikoko kama tunavyofanya kule Rufiji. Kwa hiyo, tunaendelea kutafuta fedha nyingi kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mchango wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa Zanzibar, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha na Mheshimiwa Ali Hassan Omar King wameongelea, hii ndiyo dhamira yetu. Ule mradi aliouongelea Mheshimiwa Shamsi nimechukua mawazo yale na tutaupanua na kuukuza. Shida kubwa ya wavuvi wadogo ni kuweza kufika mbali. Kwa hiyo, ili uwasaidie, usiwasadie kwa namna ambayo wataendelea kufika pale pale karibu. Kwa hilo, tumelichukua na tutalifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunaamini kwamba mchango wa Tanzania Bara kwa maendeleo ya Zanzibar siyo wa Serikali peke yake bali hata mfumo wa uchumi unaowezesha biashara kubwa zaidi na rahisi zaidi kwa pande zote mbili ili Zanzibar uchumi wake uhamasike zaidi kutokana na kuwa karibu na sehemu yenye uchumi mkubwa zaidi. Kwa hiyo, tutaendelea kushirikisha wenzetu wataalam wa biashara na uwekezaji ili tuweze kukamilisha hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano is a fact of life yaani lazima tukubaliane wote hapa na hata kama hukubali na kama viongozi lazima tuwe honest kwamba hatuna namna nyingine zaidi ya Muungano. Mwingiliano ni mkubwa, ni wa muda mrefu na gharama ya kuuondoa ni kubwa zaidi kuliko juhudi tunazoweza kuzitumia kuzirekebisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani uwekezaji kwenye kuimarisha Muungano ni muhimu zaidi kuliko tafakuri ya namna tunavyoweza kuachana. Kwa hiyo, napenda juhudi za wanasiasa wa pande zote mbili ziwe katika kuuimarisha Muungano huu. Mnanifahamu mimi ni mtu ambaye sina tatizo na mawazo ya aina yoyote na hakuna hoja inaweza kutufarakanisha au kututenganisha kwenye Muungano. Kwa hiyo, siasa nzuri zaidi ndugu zangu siyo siasa ya kuubeza Muungano ni ya kujenga, siasa nzuri zaidi siyo ya kuupa jina baya ili uhalalishe kuumong’onyoa. Siasa nzuri ni kuupa hadhi yake unaostahili ili tuweze kuwekeza katika juhudi za kuuimarisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ally Saleh amesema kwamba utaratibu wa kutatua kero haufai, lakini nitaka nimwambie tu kwamba utaratibu huu wa tangu mwaka 2006 ndiyo umetupunguzia kero kutoka 15 mpaka tatu sasa hivi. Kwa hiyo, ndugu yangu kama kuna mawazo ya utaratibu bora zaidi sisi tuko wazi kabisa na mimi nipo tayari kupokea mawazo kuhusu utaratibu bora wa kushughulikia kero za Muungano kwa sababu nchi hii ni yetu sote na mawazo bora zaidi ya kuimarisha Muungano ofisi yetu inayapokea. Kwa hiyo, tupendekeze tu kama yapo mawazo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamezungumza kuhusu kukauka kwa mito, vyanzo vya maji na maziwa, ni kweli. Katika ziara zangu nchini nafanya makusudi kutembelea vyanzo vya maji, maziwa na mito. Nimetembelea Ziwa Tanganyika, Ziwa Jipe, Chala, Natron, Manyara, Eyasi na nimejionea mwenyewe jinsi gani tunavyoelekea kwenye kuangamia.
Waheshimiwa Wabunge, ninaposema kuelekea kuangamia ninamaanisha hivi, ukienda kule Jipe utaona zile jamii za pale hata aina ya samaki wanazovua ni visamaki vidogo, mtu akitaka kwenda kuvua ni lazima apite kwenye magugu yaliyojaa kwenye ziwa. Lile ziwa nusu liko upande wa Tanzania na nusu liko upande wa Kenya. Ukipiga picha ziwa lile utaona upande wa Tanzania ndiyo kumejaa magugu, upande wa Kenya kuna hoteli pembeni ya ziwa watu wanaogelea, hii ni aibu kubwa kwa nchi yetu na hii tunafanya wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais tumeamua kwamba tutaanzisha mradi mkubwa kabisa wa kitaifa wa kutunza maziwa madogo madogo katika nchi yetu. Nimewaambia kabisa wataalam wa Wizara nitawapa likizo ya wiki tatu wakakae mahali waandike mradi wa maziwa madogo nane hapa nchini na namna tunavyoweza kuyahifadhi. Kwa hiyo, tutawaletea taarifa hiyo tutakapokuwa tumekamilisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie hali ya uharibifu wa vyanzo vya maji ni kubwa sana tutapoteza mito katika nchi hii. Waheshimiwa Wabunge, naomba niseme, watoto na wajukuu zetu watakuja kutushangaa sisi tulikuwa ni watu wa namna gani ambao tulikuwepo na kushuhudia na kuwezesha upoteaji wa kitu kama mto, unawezeshaje mpaka mto upotee? Kwa hiyo, ngoja niishie hapo nisije nikasema maneno mabaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu NEMC, Waheshimiwa Wabunge wamesema kwamba kuna haja kubwa ya kujenga uwezo wa NEMC na hilo tunalifanya. Ni taasisi ambayo imepewa mamlaka makubwa lakini uwezo wake wa kitaasisi na fedha hauendani na majukumu iliyopewa na sheria. Kwa moja ya kazi yetu sisi ni kujenga uwezo wa taasisi hii ili iendane na hadhi na heshima ya taasisi yenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye nchi nyingine Mkurugenzi Mkuu wa NEMC analindwa kutokana na kazi kubwa anayoifanya. Nchi hii Mkurugenzi Mkuu wa NEMC anaweza akapita kantini hata hujui ni nani wakati ni taasisi kubwa yenye mamlaka makubwa kabisa inayoweza kuzuia hata ndege zisiruke kwa sheria hii. Mkurugenzi Mkuu wa NEMC anaweza akasema Emirates isiondoke mpaka nijihakikishie kwamba haivujishi mafuta, ndiyo nguvu ya kisheria ya taasisi zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi moja ya majukumu yetu tangu tulipoingia Wizarani ni kujenga uwezo wa kitaasisi, ndiyo maana tumefufua Mfuko na Baraza la Rufaa. Watu wa NEMC mkiongea nao watawambia, NEMC tuliyoikuta na NEMC ya sasa kama alivyosema Naibu Waziri ambayo ilikuwa inakusanya shilingi bilioni 5 sasa hivi 12 ni tofauti. Kazi hiyo itaendelea na katika siku chache zijazo mtasikia kazi tutakayoifanya NEMC ya kubadilisha mambo pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mzee wangu Mheshimiwa Nsanzugwanko ananiangalia sana nataka niseme jambo lake, mwaka jana wakati tunawasilisha bajeti hapa, Mheshimiwa Nsanzugwanko na Mheshimiwa Bilago walisimama na kushika mshahara kwa kusema kwamba hatujazungumza lolote kuhusu uharibifu wa mazingira unaofanywa na wakimbizi. Nataka niwaambie kwamba baada ya lile jambo mimi nikafanya safari kwenda kwenye kambi za wakimbizi, bahati mbaya sikusema kwenye hotuba na nikatembelea Nyarugusu, Makere, Mtabila na vijiji vyote vinavyozunguka kambi za wakimbizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikawaita wakuu wote wa UNHCR kule Kigoma na nikawapa maelekezo yafuatayo siyo kwa mdogo ni kwa barua. Kwanza, makambi yote ya wakimbizi Tanzania yafanyiwe EIA. Sheria yetu inasema, maeneo ya makazi makubwa lazima yawe na environmental impact assessment lakini nilistajabishwa kwamba makambi yale yalikuwa hayana environmental impact assessment. Kwa hiyo, kwanza tukawapiga faini kwamba hawakuwa na EIA lakini pia tukawalazimisha wafanya EIA ambayo itatoa masharti ya matumizi ya eneo lile ikiwemo hifadhi ya mazingira, hilo ni agizo la kwanza nililowapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, agizo la pili nililowapa, ni kwamba walikuwa na pilot project ya kuwapa majiko ya gasi wakimbizi. Tukasema kwanza isiwe pilot iwe ni mradi, lakini usiishie kwa wakimbizi bali uishie pia kwa jamii inayozunguka kambi hizo ili wasikate kuni. Agizo la tatu nililowapa ni kwamba wachangie kwenye miradi ya maendeleo katika vijiji vinavyozunguka makambi ya wakimbizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, najua alininong’oneza kwamba atashika tena mshahara lakini naamini taarifa hii itamridhisha na ataachia mshahara wangu kwa sababu kazi tumefanya na tunafuatilia. Ulinituma na nimeenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ulisema kwamba Kasulu kuna tatizo la vyanzo vya maji na tumepeleka timu na tutaandika mradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, naomba nimalize kwa kusema kwamba kazi tuliyopewa na Taifa ya kusimamia uimara wa Muungano tunaifanya vizuri, naamini kabisa kwamba katika kipindi cha mwaka mzima uliopita, hamjasikia kelele, malalamiko kuhusu Muungano kama mlivyokuwa mmezoea kusikia siku za nyuma. Hili jambo halijatokea kwa ajali kwamba watu wamelala ni kwamba kuna kazi imefanyika ya kuhakikisha kwamba tunapunguza kero na malalamiko. Muungano na jina baya la Muungano halipo tena kwenye vichwa vya habari. Hii siyo kwa sababu akina Mheshimiwa Ally Saleh wanachapana bakora kule hapana, hii ni kwa sababu tumefanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia wote mnafahamu kwamba hifadhi ya mazingira kama alivyosema Naibu Waziri na Mwenyekiti imeongezeka na tutaendelea kufanya kazi kubwa, naomba muendelee kutuamini na kutuwezesha. Kama mnavyojua sisi ni rafiki wa watu wote na kwa maneno hayo, nategemea hatutapata shida sana kwenye kupitisha bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru wote waliochangia na naomba kutoa hoja.
Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MAZINGIRA NA MUUNGANO): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru tena, lakini pia naishukuru Kamati kwa maoni mazuri waliyoyatoa na ushauri tutauzingatia wote. Pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Ally Saleh Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani kwenye masuala ya Mazingira na Muungano. Bahati nzuri yeye ni mwanamazingira mzuri, ametoa mawazo mazuri na tutayazingatia hasa la kushirikisha wadau zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika,ia suala la baadhi ya vipengele ambavyo vimezungumzwa kwa ujumla na hakuna ufafanuzi kuhusu utekelezaji wake. Nataka nimweleze tu kwamba majadiliano bado yanaendelea kuhusu namna ya utekelezaji wa makubaliano haya. Kwa hiyo, mambo mengine aliyoyazungumza yatapatiwa majawabu na ufumbuzi mara pale mazungumzo kuhusu utekelezaji wa mkataba huu yatakapokwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kujibu karibu mambo yote yaliyozungumzwa na kwa kwa ufasaha kabisa na kwa kweli zaidi ya hapa nampongeza, mwanzo nilisahau kumshukuru kwa mchango wake na kazi nzuri anayoifanya katika ofisi yetu ili kusaidiana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Lubeleje amezungumza kwa hisia sana kuhusu masuala haya na namshukuru. Wakati mwingine utu uzima unasaidia kuonesha tofauti. Asilimia 50 ya Watanzania ni watu wa umri wa chini ya miaka 18. Asilimia 44 ya Watanzania ni watoto chini ya miaka 14. Kwa hiyo, unapokuwa na Taifa la watu wengi ni wenye umri mdogo, wanakuwa hawajapata kuona nchi ilikuwaje miaka iliyopita na ilivyo sasa. Kwa hiyo, wanaona huu uharibifu uliopo na hali iliyopo sasa ndivyo nchi ilivyo, kwa hiyo, wanakosa uchungu na hamasa ya hifadhi ya mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mzee Lubeleje, amekula chumvi nyingi na anaposema hasa kwamba miaka ya 1960 nchi hii haikuwa hivi, ni kweli, ana ushuhuda kwa sababu ameona ilivyokuwa huko. Kwa kweli tungependa yeye na wazee kama yeye wapate nafasi hizi za kutuelimisha sisi vijana, tuone kwamba uoto wa asili na landscape ya nchi yetu, kwa kweli inaharibika kwa haraka sana katika miongo hii kadhaa aliyoishi, ambayo vijana wengi wa sasa wataishi, hali itakuwa mbaya zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunamshukuru sana kwa ushuhuda wake. Kama nilivyomwelekeza Naibu Waziri, atakwenda Jimboni kwake. Kwa kweli hali ni mbaya, ndiyo maana tumepeleka huu mradi mmoja Jimboni kwake kwa ajili ya kusaidia watu wa Mpwapwa. Nafahamu kuna habari ya makorongo mengi yanayopitisha maji na kuharibu mazingira na Naibu Waziri atakuja kuyaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Mheshimiwa Salum, amezungumza kwa hisia sana na kwa kweli ametufundisha na kutueleza jinsi gani baianuai inavyopotea. Kwenye kisiwa kama cha Zanzibar ambapo eneo ni dogo na utajiri wa Zanzibar; utajiri wa Tanzania kwa kweli haupo chini ya ardhi peke yake kwa maana ya madini. Utajiri ni kwenye maarifa ya Watanzania lakini pia ni kwenye uoto na mimea na wanyama ambavyo Mungu ametujaalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya nchi hapa duniani zina aina chache sana za mimea, aina chache sana ya wanyama, ndiyo maana wanakuja huku na dunia inavyoenda kuna baadhi ya nchi hata sauti ya ndege watoto wanaozaliwa miaka inayokuja watakuwa hawaijui mpaka waje kwetu. Sasa na sisi tukipoteza ndege wale, ina maana vizazi vijavyo tutakuwa tunahadithiana kwamba, bwana kuna ndege fulani aliishi miaka hiyo alikuwa na rangi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, utajiri mkubwa kabisa wa nchi yetu ni baianuai (bio-diversity); wingi wa mimea na wanyama. Sasa huu mkataba tunaouzungumza leo, makubaliano haya yapo chini ya makubaliano ya UNFCC United Nations Convention of Climate Change na siku ile yale makubaliano yalivyowekwa sahihi kule Brazil kulikuwa na mkataba mwingine unaitwa Mkataba wa Uhifadhi wa Baianuai (Convention on Biological Diversity) ambao sisi ni wanachama wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, ule mkataba unatoa fursa nyingi za kuhifadhi baianuai. Pia unatoa nafasi ya nchi yetu kutajirika na kunufaika na baianuai yetu tuliyonayo. Baianuai siyo kwa maana tu ya kuja kuitazama, lakini kuitumia kwenye tiba, utafiti na kadhalika. Mnafahamu madawa yote yanatokana na miti; na mnapoharibu miti na mimea mnapunguza uwezo wa kujitibia siku zijazo. Kwa hiyo, uharibifu wa mazingira ndugu zangu unahusu pia hata tiba yetu kwa miaka inayokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashukuru kwamba hilo tumelizungumza na sisi kama Serikali, tunaendelea na utekelezaji wa mikataba yote hii miwili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana Mheshimiwa Mbunge amezungumza kwamba tubadilike. Leo tunazungumza mabadiliko ya tabianchi lakini inawezekana cha kwanza kinapaswa kuwepo ni mabadiliko ya tabiamtu ili tuweze kudhibiti mabadiliko ya tabianchi. Kwa sababu kama mabadiliko ya tabiamtu hayatokei, itakuwa ni vigumu sana kudhibiti mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumezungumzwa pia kuhusu kuni na mkaa na Mheshimiwa Mbogo vile vile amezungumza kuhusu kuni na mkaa. Nataka nizungumze kwamba sisi tunaangalia matumizi ya nishati hizi za tungomotaka wanaita (biomass) katika suala zima la deforestation na landscape degradation, kwamba huu uoto unaouona, ardhi, mimea; hii landscape ya nchi yetu inayopendeza, kasi yake ya kuharibika ni kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo, ufugaji, utalii maji, zote zina uhusiano na hifadhi ya mazingira. Kwa hiyo, tunapopata uharibifu wa landscape, huu uoto, hizi sekta nyingine zote haziwezi kufanikiwa. Kwa hiyo, uchumi wa nchi yetu na ukuaji wa uchumi na umaskini na ustawi wa watu, unafungama moja kwa moja na hifadhi ya mazingira. Huwezi kutofautisha!

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi tunasema hapa, tunataka kuhamasisha Wabunge wote wawe wanamazingira. Kama unataka kuzungumza maji Jimboni kwako, huwezi kuyapata bila hifadhi ya vyanzo vya maji, bila hifadhi ya miti na kadhalika. Kwa hiyo, nafurahi kwamba waliochangia karibu wote wamesaidia kutoa elimu na wamesaidia kuonesha hisia katika mambo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwenye matumizi ya kuni na mkaa, sisi kama Serikali tunashirikiana na tutashirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii kuhakikisha kwamba tunatengezea mpango mkubwa wa Kitaifa wa matumizi ya nishati. Tayari maelekezo yametolewa kwenye Wizara ya Nishati na Madini kutunga sera mpya ya nishati ya tungomotaka (biomass policy) ili tuwe na mwongozo wa namna gani tunapata nishati ya kupikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi kinachotokea ni kwamba miti iko vijijini lakini ukataji wake unanufaisha watu wa mijini. Watu wa mjini hawana miti, lakini watu wa vijijini kuni zile wanakata matawi tu. Ili mtu wa mjini apate mkaa, ni lazima akate mti wenyewe, gogo lile. Sisi kwenye shule, Magereza na Mahospitali, hatutumii kuni za matawi tu, ni lazima tukate mti wenyewe. Ukienda unakuta lundo la magogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais tumetumia kifungu cha 13 cha Sheria yetu ya Mazingira ambacho kinasema kwamba Waziri mwenye dhamana ya mazingira ana uwezo wa kuelekeza mamlaka zozote za kisekta, binafsi na taasisi kufanya mambo ambayo yatahifadhi mazingira. Kwa hiyo, tumetoa maelekezo kwa shule, Magereza, hospitali na tumewapa mwaka mmoja kwamba waondokane na matumizi ya kuni na mkaa na tumeanza hapo UDOM.

Mheshimiwa Naibu Spika, UDOM pale pana wanafunzi takriban 30,000, wanapikiwa chakula mara tatu kwa siku. Sasa hebu fikiria kulisha watu 30,000 mara tatu kwa siku, kiwango cha kuni kinachotumika ni kikubwa sana. Ukienda pale utataka kutoa machozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wale tumewaambia ndiyo watakuwa wa kwanza na bahati nzuri tumekubaliana kwamba watu wanaowapa zabuni pale, wote sasa ili upate zabuni ya kupika chakula, hauwezi kupata kama unatumia mkaa au kuni. Kwa hiyo, tutaona mabadiliko yaliyotokea pale UDOM yatatusaidia kutoa mfano kwenye taasisi hizi kubwa zenye watu wengi kuhusu kuondokana na hili suala.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili ni jambo ni kubwa, sisi kama Serikali tunalichukulia kwa uzito wake. Matumizi ya nishati nchini yanafungamana na umaskini kwamba masikini zaidi ndio wanagharamia nishati zaidi. Pia tusisahau kwamba wewe unatoka Pemba; ukitazama mkaa unaopelekwa Pemba kutoka bara, haulingani na idadi ya watu walioko Pemba.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kule kwenye hizi bandari za kwetu; Mbweni, Bagamoyo utaona magunia ya mkaa yanaenda Pemba. Unajua yanaenda wapi? Hayaendi Pemba, yakifika Pemba yanaenda shimoni, Mombasa. Yakifika Mombasa yanapakiwa vizuri yanaenda Somalia au Uarabuni kuchoma kondoo vizuri. Maana wale wanataka kuchoma kondoo na mkaa mzuri; na yakienda Somalia yanasaidia ku-finance Al-shabaab.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mkaa wetu tunaweza tukauona hapa ni jambo la kawaida lakini una muunganiko na value chain kubwa sana ambapo wote kama Serikali na Wizara ya Maliasili na Utalii ambayo ndiyo inahusika moja kwa moja na haya mambo, inabidi tukae tupange vizuri. Kwa sababu siyo tu kwamba mkaa unaokatwa nchini unatumika nchini, unaenda nje ya Tanzania vile vile. Kwa hiyo, tunakata miti yetu sisi kwa manufaa ya watu wengine huko nje ya Tanzania. Kwa hiyo ni suala la kulizungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia matumizi bora ya ardhi. Moja ya changamoto kubwa inayosababisha sisi tushindwe kuhimili mabadiliko ya tabianchi ni kwamba tuna kilimo hiki cha kuhamahama. Mtu anavamia msitu, analima mtama misimu miwili, ardhi ikiharibika anakata tena kipande kingine cha msitu. Kwa hiyo, baada ya miaka michache unakuta msitu wote umefyekwa. Au wale wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sisi kama nchi, wajibu wetu ni kuweka taratibu za kutumia vizuri ardhi. Kielelezo na shabaha ya maendeleo ni kutumia ardhi kidogo kuvuna zaidi. Nitatoa mfano, nchi ya Uholanzi, eneo lake ni dogo kuliko Mkoa wa Katavi, yaani Mkoa wa Katavi ni mkubwa kuliko Uholanzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Uholanzi ni nchi ya pili duniani kwa kuuza bidhaa za kilimo pamoja na kuwa na eneo dogo. Ukiondoa Marekani, inakuja Uholanzi. Uholanzi wanauza dola bilioni 90 za mazao ya kilimo kwenye eneo kama la Mkoa wa Katavi. Kwa hiyo, ndiyo kielelezo cha maendeleo. Nasi tunaweza kufika huko. Wanafanya hivyo bila kutumia GMO wala nini, ni kilimo tu endelevu na wanahifadhi mazingira na ni kuzuri. Kwa hiyo, naamini maendeleo yetu yatafikiwa tutakapokuwa tumefanya mambo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbogo nashukuru sana kwa mchango, nimekupata. Tutashirikiana na Serikali za Mitaa na tumezungumza na wenzetu wa Wizara ya Fedha, Naibu Waziri yupo ananisikia, tumependekeza kwamba kila Wizara na kila Halmashauri iwe na budget code yaani zile…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri, naomba urudi ukae kidogo.....

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kutoa pendekezo kwamba, saa yetu ile pale mbele itengenezwe. Kumbe inakuwa sahihi mara mbili kwa siku. Naona imesimama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasema kwamba, kuhusu mapendekezo ya Mheshimiwa Mbogo kuhusu ushirikishwaji wa Halmashauri na viongozi kwenye maeneo yetu ya vijiji, Wilaya na Halmashauri tutayachukua, tumeyazingatia.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya mipango yetu katika Ofisi yetu ya Makamu wa Rais ni kufanya kazi kwa karibu zaidi na Serikali za Mitaa. Katibu Mkuu anayo maelekezo yetu kuandaa mikutano baina ya ofisi yetu na Serikali za Mitaa kwenye level ya Mawaziri, Makatibu Wakuu, lakini pia kujaribu kutumia fursa za vikao mbalimbali vilivyopo ikiwemo vikao vya RCC ili kuweza kwenda kutoa elimu kwao, lakini kuweka makubaliano ya ushirikiano ikiwemo ushirikiano katika kuhakikisha kwamba Sheria ya Mazingira inazingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata baadhi ya masuala ikiwemo ya usimamizi wa sheria, ikiwemo ya kufanya hizi habari za tathmini ya athari kwa mazingira, baadhi ya mambo tunafikiria kuyakasimu kwenye Serikali za Mitaa. Kwa hiyo, mpango huo upo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema awali kabla sijakaa, itapendeza kama tutakubaliana ndani ya Serikali kuwa na budget code, ili kila Halmashauri katika bajeti yake iwe na sehemu inasoma namba zile, “Hifadhi ya Mazingira,” ili fedha ziweze kupangwa kwa ajili ya hawa Wakuu wa Wilaya, kama ulivyosema, wapate OC ya kuzunguka na kusaidia kwenye hifadhi ya mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kupanda miti, Naibu Waziri amelizungumza kwamba tutalipa msukumo mpya na tutafanya sensa ya miti. Pia, niseme tu kwamba, kama tulivyozungumza kwenye Azimio kwamba pale Morogoro tumeanzisha kituo kinaitwa National Carbon Monitoring Centre ambapo kuna teknolojia ya kujua kasi ya uharibifu wa mazingira maeneo ambayo miti inahitaji kurejeshwa. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri wa Maliasili ni mhusika pia kuhusu masuala ya misitu, kwa hiyo, tutashirikiana naye kuhakikisha kwamba tunafanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa zaidi kuhusu misitu, siyo kupanda miti mipya, ni kutokata iliyopo. Katika miti yote iliyopo Tanzania, 95% ni ile iliyokuwepo, 5% tu ndiyo iliyopandwa. Kwa hiyo, ili ufanikiwe zaidi kwenye hili jambo, usikate miti, bali uhifadhi ile ambayo haijakatwa na hiyo itatusaidia tutakapowezesha watu kutotegemea miti zaidi katika maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Kamala kwa hoja nzuri alizoziwasilisha za sababu ya kuunga mkono. Tunakushukuru na tunakubali kwamba sisi kuridhia haya makubaliano kutatusaidia kuweza kupata fursa. Zaidi tunafurahi kwamba yeye kama Mbunge, anaona haja ya Serikali kuwa na rasilimali nyingi zaidi na Bunge mna wajibu pia wa kupanga fedha kwa ajili ya hifadhi ya mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa fedha kwa ajili ya hifadhi ya mazingira haziko kwenye bajeti peke yake, ziko namna nyingi ikiwemo Mfuko wa Taifa wa Dhamana ya Mazingira ambapo kwenye sheria ile unategemea moja ya vyanzo vilivyoandikwa vya Mfuko, nacho ni subvention appropriation kutoka kwenye Bunge, ukiondoa kwenye bajeti. Kwa hiyo, Bunge lina uwezo wa kuamua lenyewe kwamba licha tu ya bajeti ya Serikali kwa Ofisi ya Makamu wa Rais, pia tunaweza kabisa kupangia Mfuko wa Mazingira kiasi fulani cha fedha na Mfuko huu utakapopata fedha hizo, basi utatuwezesha kufanya kazi zetu vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, nadhani nimeweza kuzungumza yote yaliyozungumzwa, lakini niseme tu kwamba, ushauri uliotolewa tutauzingatia. Tunaomba sasa utusaidie namna ya kwenda kwamba, tunatoa hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na taadhima, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa uliyonipa ya kuhitimisha hoja hii. Nianze kwa shukrani kwa Kamati zote kwa maoni, ushauri, mapendekezo waliyoyatoa. Pia nawashukuru Waheshimia Wabunge wote waliochangia idadi yao ni 45; Wabunge 30 walichangia kwa maandishi na Wabunge 15 walichangia kwa mdomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo ni mengi na niseme tu kama alivyosema Naibu Waziri kwamba kama hatutayafikia yote, basi kwa ujumla kabla ya mwisho wa Bunge hili la bajeti, tutawawekea kwenye pigeon holes zenu majibu ya maswali yote mliyouliza. Hata hivyo, nizungumze mambo ya jumla ambayo yamezungumzwa na kubwa ni lile la kwanza la masuala ya biashara, vikwazo vya biashara na kwamba imetolewa kauli hapa na baadhi ya Wabunge ambayo kwa kweli sisi kama Serikali ni lazima tuielezee vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli yenyewe ni kwamba, baadhi ya wachache ni kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano haina dhamira ya kuisaidia Zanzibar kiuchumi na kwamba inabana fursa za biashara na ukuaji wa uchumi wa Zanzibar sasa kauli kama hiyo haiwezi kubaki bila kutolewa maelezo na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme tu kwamba, kihistoria hata kabla ya mapinduzi, hata kabla ya uhuru, miaka mingi iliyopita, mahusiano kati ya bara na Zanzibar msingi wake mkubwa ulikuwa ni biashara na hata kabla Serikali hizi mbili hazijaundwa na kwa kweli Muungano umekuja kurasimisha tu mambo yaliyokuwepo tayari. Uhusiano mkubwa kabisa na mzuri kabisa wa kibiashara watu wengi wa bara ambao wamekuwepo Zanzibar miaka mingi kwa sehemu kubwa walienda kule kwa sababu ya biashara na watu wa Zanzibar wengi waliokuwa wamekaa bara kwa vizazi na vizazi sababu kubwa iliyowaleta ilikuwa ni biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa fursa za biashara tunazoziongea sasa hivi ziko kwa namna mbili; kwanza, ni uwezo na urahisi wa kusafirisha bidhaa kati ya pande zote mbili, hiyo ni namna moja na ndiyo ambayo imechukua sehemu kubwa ya mjadala. Namna ya pili, ni uwezo na urahisi wa mtu yeyote kutoka upande wowote kwenda kuishi upande wowote kwa urahisi zaidi na kuanzisha biashara hiyo ni namna ya pili ambayo haikuzungumzwa sana lakini ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tunafahamu kwamba hii ya pili, uwezo wa mtu yeyote kwenda upande wowote wa Muungano kutengeneza makazi, kutengeneza maisha na kufanya biashara huu pia umekuwa msingi mkubwa wa uimara wa Muungano wetu na maingiliano yetu. Sidhani ndiyo maana haikuzungumzwa, kwa sehemu kubwa kabisa, tunapotafakari kuhusu mchango na hatua za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwezesha ukuaji wa uchumi na ustawi wa watu wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili pia ni muhimu kulitazama; je, ni rahisi zaidi kwa mtu kutoka Zanzibar kuja bara kupata mahali kuanzisha biashara na kushamiri na kusaidia nyumbani Zanzibar? Jibu ni ndiyo, ni rahisi na kwa nini ni hivyo? Ni kwa sababu ya Muungano. Kwa hiyo, huwezi kuuondoa Muungano katika ustawi wa watu wa Zanzibar unaotokana na urahisi wa watu wa Zanzibar kuja Bara na kufanya biashara na kushamiri. Kwa hiyo, hiyo ni manufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili la pili na hili ni jambo jema kabisa na tunataka iendelee kuwa hivyo. Tunafurahi kuona Wazanzibar wengi zaidi wanakuja kuishi bara na kustawi na kusaidia Zanzibar na Wazanzibari walioko bara sasa hivi ni wengi zaidi kuliko Wazanzibari wote waliko Kisiwa cha Pemba. Miaka 20 au 30 ijayo, Wazanzibari kwa mwenendo tunaokwenda, Wazanzibari wanaoishi Bara wanaweza kuwa wengi kuliko Wazanzibari wote walioko Zanzibar na hilo ni jambo jema, ndiyo Muungano na tunaoutaka na ndiyo fursa na muingiliano sahihi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani kwamba katika mazungumzo tunayozungumza hapa kuhusu ustawi wa Muungano wetu tusisahau uzuri na ukubwa wa fursa inayotokana na urahisi wa Wazanzibari kuja kufanya biashara bara. Wote tunajua kwamba katika maeneo yetu hasa ya Pwani, sisi tunaotoka Tanga, tunaotoka Dar es Salaam na kwingineko na hata katikati ya nchi yetu huwezi kwenda maduka mawili, matatu bila kukuta duka la Mzanzibari ambaye anafanya kazi na ananufaika na anasaidia Zanzibar hivyo hivyo. Kwa hiyo, kikubwa tu tunaomba kwamba wakija huku pia tujue wote ni raia wa nchi moja na pia wasaidie kwenda kujenga nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili la kwanza la urahisi wa kufanya biashara, urahisi wa kupeleka bidhaa; hakuna anayebisha kwamba kuna changamoto kabisa siwezi kusimama hapa kama Waziri mwenye dhamana ya Muungano nikasema hakuna shida yoyote kuhusu bidhaa zinazokwenda kwa pande zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunafahamu kwamba kihistoria, biashara kati ya pande zote mbili haikuwa rasmi sana na baada ya sisi kuunda Serikali, kufanya Muungano na katika historia ya maendeleo ya uchumi wa nchi yetu na biashara, kumetokea hatua mbalimbali za kurasimisha uchumi na biashara na zile hatua zililazimika kuunda Taasisi mbalimbali na baadhi ya Taasisi hizo ni Taasisi za udhibiti zikiwemo TFDA, ZFDA, TBS, ZBS, sasa TRA ambayo haikuwepo mpaka mwaka 1996 ndiyo ilianzishwa TRA.

Sasa katika utendaji kazi katika hizi mamlaka na mamlaka ikishaitwa ya udhibiti wakati mwingine lile neno udhibiti linapitiliza mipaka. Inadhibiti siyo kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri bali inadhibiti hata kuhakikisha mambo yenyewe yanafanyika. Kwa hiyo, sisi tunafahamu kwamba sasa hivi tunapitia kipindi cha tunaweza kusema readjustment ya hizi mamlaka kufahamu wajibu wake na kufahamu kwamba zina wajibu wa kusaidia masuala ya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa imezungumzwa hapa kwamba nilifanya ziara mahususi kule Zanzibar mwezi wa Oktoba na hili suala la biashara na vikwazo vya biashara, sisi Serikali tulianza kulifanyia kazi kabla halijazungumziwa Bungeni hapa. Nimeenda Zanzibar, mkutano wangu wa kwanza mkubwa kabisa tulikuwa na Zanzibar Chamber of Commerce ambao kulikuwa na mamlaka nyingine na Taasisi zingine pale za wafanyabiashara kama vile Zanzibar Freight Bureau, Zanzibar Exporters Association na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikutana na wafanyabiashara wanaohangaika kufanya biashara kila siku kati ya Bara na Zanzibar na wakanieleza kwa kina na kwa umahiri mkubwa jinsi biashara kati ya Bara na Zanzibar inavyofanyika na changamotozo zilizopo katika biashara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukazungumza structure ya uchumi wa Zanzibar kwamba kwa sehemu kubwa ni service oriented, utalii na biashara na structure ya uchumi wa Bara ambao kwa sehemu kubwa ni diverse; kuna madini, kuna kilimo, kuna ufugaji, kuna uvuvi na kadhalika na kwamba currency ya nchi yetu ambayo pia inasaidia wafanyabiashara wa Zanzibar kuagiza bidhaa kutoka nje, stability yake inategemea na mix kati ya hizi chumi mbili ambazo lazima ziwe interdependent, lazima ziwe zinategemeana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hata ustawi wa uchumi wa Zanzibar vilevile kwa kiasi kikubwa unategemea diversity ya uchumi wa Bara kwamba sisi na hata control ya inflation ya Zanzibar inategemea stability ya currency inayotokana na diversity ya uchumi wa Bara. Kwa hiyo, haya mambo lazima yatazamwe katika upana wake na tukazungumza na wafanyabiashara kuhusu hayo mambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nikafanya ziara bandari ya majahazi na mahali kwingineko, tukazungumza kuhusu ughali wa kuleta mizigo Zanzibar kutoka siyo tu Bara bali kutoka kote duniani na ni kwa namna gani tutarahisisha uagizaji wa Zanzibar wa bidhaa usiwe ni through transshipment kwa Bara kwamba mzigo unashushwa mahali kwingine ndiyo unachukuliwa na majahazi au meli ndogo kuja Zanzibar. Ni kwa kiasi gani Zanzibar inaweza kuagiza mzigo directly yenyewe moja kwa moja kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikafanya ziara TRA kwa upande wa Zanzibar, ZRB, Mamlaka ya Bahari Kuu, nikakutana na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na vijana na tukakusanya mambo yote ambayo yanawakwaza Wazanzibari kuhusu biashara na tarehe 23 Oktoba, nikakutana na Waziri wa biashara wa Zanzibar, Mheshimiwa Amina Salum Ally na jopo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nilimwomba Waziri Ummy anipe mtu wa TFDA na Waziri Mwijage anipe mtu wa TBS ili wawepo kwenye ule mkutano, tukapitia hoja moja mpaka nyingine inayosababisha watu wa Zanzibar iwe vigumu wao kufanya biashara na tukazichukua zile hoja, tukazitengenezea matrix.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 27 Oktoba, tukamuomba Mheshimiwa Makamu wa Rais atuite wote, Wizara ya Fedha Zanzibar, Wizara ya Fedha ya Muungano, Wizara ya Biashara ya Zanzibar na mamlaka zote za udhibiti mpaka TRA tukapitia hoja moja bada ya nyingine ya vikwazo vya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Biashara akaelekezwa kwamba aende na wataalam wake Zanzibar akakutane na Waziri mwenzake wapitie hoja moja baada ya nyingine na kikao hicho kikafanyika tarehe 22 Machi na matrix hapa ninayo na mambo yote yaliyoorodheshwa ikiwemo ya VAT, ikiwemo hizi Mamlaka mengine yalitatuliwa katika mchakato huu na mengine yataendelea kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilikutana na Waziri wa Fedha wa Zanzibar ambaye alieleza masuala ya biashara kwa upande wa fedha. Kwa hiyo, baada ya kueleza hizi jitihada ambazo tumefanya sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kukutana na wafanyabiashara kwa makundi na mmoja mmoja, kukutanisha sekta, mimi kukutana kama Waziri wa Muungano na Waziri wa Biashara inaniuma sana akisimama Mbunge akisema Serikali ya Jamhuri ya Muungano haina dhamira ya kutatua changamoto za biashara kwa upande wa Zanzibar, kwa sababu najua kabisa kazi ambayo tumeifanya na siyo sahihi kabisa kusema hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na inawezekana hatuna uhodari sana wa kuyatangaza haya mambo ambayo tunayafanya, lakini kwa kweli tunayafanya. Naomba sana Waheshimiwa Wabunge tusaidiane mawazo hapa, nini zaidi yatulichofanya kinafaa kufanywa zaidi na sisi tuko tayari. Nimesikitika kwamba wakati baadhi ya Wabunge wanaeleza shida zilizopo na hizo shida zinathibitishwa na Wabunge wengine kunakuwa na makofi ya kufurahia kwamba shida zile zimekuwa confirmed.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani siyo sawa, tusifurahie kunapokuwa kwamba tume-confirm, nadhani kuzomea na kuzodoa ni rahisi zaidi kuliko kushauri, lakini kazi yetu ni kushauri na sisi tuko tayari kupokea ushauri wowote ambao utasaidia tuondoe haya mambo kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge muamini kabisa kwamba suala la biashara kati ya Tanzania Bara na Zanzibar, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inalijua, imelishughulikia na inaendelea kulishughulikia. Nimetengeneza marafiki wengi sana wafanyabiashara wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ziara yangu na nimekutana nao akina Mohamed Masoud Rashid, Omar Hussein Mussa, Abdallah Abbas Omar, Wakili Awadh Ally alikuwepo kwenye mkutano na kuna baadhi ya mambo tuliyashughulikia pale pale, wale waliniambia kwamba Benki Kuu imetoa waraka kwamba minimum ya kiwango cha bureau de change ni milioni 300 na kwamba bureau de change za Zanzibar ni ndogo ndogo wanaomba tusaidie kwa upande wa Zanzibar kufanyike exception na tulifanya. Tulimpiga simu Governor Ndullu akasema ataenda. Kwa hiyo wakati mwingine haya mambo tunayafanyia kazi wakati huo huo tukiwa kwenye ziara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mikopo alizungumza Ndugu Jamal na ningependa kujibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu terminal two, ni kweli kumekuwepo na changamoto pale ya extension kuongeza mkopo mwingine kwa ajili ya kumaliza lile jengo na limekuwa ni jambo kubwa la lawama wakati anazungumza watu wakapiga makofi kwamba ni kweli kabisa mkopo umenyimwa. Hata hivyo, nataka kusema kwamba mchakato wa kutoa mikopo kwenye Serikali una hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya hatua za mwisho mwisho kabisa, ni mkopo ule kupitishwa na Kamati ya madeni ya Taifa. Kwa hiyo, nataka niwambie Mheshimiwa Jamal na Wazanzibari, rafiki zangu, ndugu zangu wapendwa kwamba mapema mwezi huu Kamati ya madeni ya Taifa ilipitisha na kukubali Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikope dola milioni 58 zaidi kwa ajili ya kumalizia jengo lile le terminal two pale uwanja wa Ndege wa Zanzibar. Kwa hiyo, jambo hilo litakwisha, litakuwa siyo hoja tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa Bandari ya Mpigeduri. Taarifa tulizonazo sisi kutoka kwa wenzetu wa Wizara ya Fedha na Zanzibar na hapa barani kwamba bado kuna maelezo ya ziada ya kitaalam na kibiashara na kuchumi yanahitajika ili kuweza kujenga hoja nzuri zaidi hata kule tunakokopa pesa, lakini Serikali ya Jamhuri haina dhamira ya kunyima uwezo Zanzibar kujitengenezea Bandari yake ambayo ni mhimili wa uchumi wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hapo hapo kuna mradi wa e-government, kuna mkopo, nadhani masuala haya ni muhimu yazungumzwe vizuri kwa sababu mikopo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayokwenda kufanya miradi Zanzibar bado marejesho ya fedha zile yanalipwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, ndiyo maana kuna ushirikishwaji mkubwa na ushirikiano mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuna miradi mingine ya maendeleo Zanzibar, hospitali ya Mnazi mmoja, SUZA, Barabara ya Chake-Wete hadi Gando kupitia mifuko mbalimbali kama vile Saudi Fund, Quwait Fund na BADEA, yote hiyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasaidia na inashiriki kuwezesha fedha zitoke ili kazi hiyo ifanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kodi na usumbufu, tumesikia na ni kweli ni changamoto. Dada yangu Tauhida nimekusikia, nakubali na nimekuelewa, nitapanda Boti ya Azam lakini nadhani MV. Mapinduzi basi siku moja nitapanda tujionee nini kinaendelea. Hata hivyo, tumeelezewa changamoto nyingi zilizopo pale na kuna mambo mawili pale yanayojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, ni kweli kwamba nchi yetu sisi vituo vya forodha vipo popote ambapo unaweza kuingia kutoka nje ya nchi ikiwemo Zanzibar na tunapaswa kuwa na mfumo wa pamoja wa forodha kwamba ukiingiza bidhaa kwenye kituo cha forodha cha Zanzibar labda umechukua gari kutoka Dubai iwe sawa na umeingiza Tanga kutokea Dubai. Yote hiyo inategemea mfumo wa pamoja wa uthamini wa kodi. Sasa tumesimika mfumo wa pamoja wa kuthamini kodi lakini hatujaanza kuutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mfumo mpya unaitwa TANSIS ambao ndiyo una database ya thamani ya bidhaa zote duniani ili kodi iweze kuthaminishwa kwa pamoja ili usilazimike kuonekana kama umelipa mara mbili, ukija Bara kumbe umelipa tofauti. Sasa ukadiriaji unaotegemea macho ya mtu, akili ya mtu moyo wake ndio unasababisha tuwe na changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo tunalijua na bahati nzuri kuna kikao tarehe 28 mwezi huu hapa na limezungumzwa sana na kuna baadhi ya mambo madogo tu ya kitaalam yamebakia ili tuwe na mfumo wa pamoja wa kuthaminisha bidhaa. Huo mfumo ukiwekwa, basi hizi shida zote zilizozungumzwa hapa zote zitakwisha, kikubwa ni hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo mengi, kwa hiyo, nipande upande mmoja wa mfumo. Upande wa pili ni watu kwamba wakati mwingine kwenye vituo hivi vya forodha kuna watu wakorofi tu ambao kazi yao ni ku-harass watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaona kabisa kwamba huyu mama ametoka Zanzibar, amefungasha khanga na kuna watu wa kutoka kule Makunduchi anakotoka Mheshimiwa Wanu, wakienda kuoa, basi wanabeba masanduku na masanduku ya khanga, kuna jina lao wanatumia, nimelisahau. Wakifika pale, unaona kabisa akinamama wa watu wamepaka hina, unaona wanaenda harusini, unaona wako kundi na wanakuelezea, lakini mtu hataki kukubali. Sasa inawezekana mtu akili hana, lakini hata macho ya kuona hana, kuona kwamba hapa hili jambo ni la wazi kabisa kwamba hawa watu ni mizigo binafsi na wala siyo biashara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili tumezungumza na wenzetu wa mamlaka ili tuwe tunaambiana. Kama kuna wafanyakazi wakorofi ambao wanawasumbua watu, basi watupe majina ili waweze kubadilishwa kwenye vituo hivyo. Mchango wa watu binafsi kwenye kuharibu mambo upo na ni mkubwa. Kwa hiyo, tunaweza tukaja hapa tukalalamika sana kumbe ni mtu tu utashi wake kwenye kusumbua watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine ni mambo makubwa sana yanatokea. Nitatoa mfano wa jambo moja ambalo tumelishughulikia ambao ulikuwa ni uamuzi wa mtu mmoja tu. Zanzibar inapata watalii wengi kutoka Italia, nadhani nusu ya watalii wa Zanzibar wanatoka Italy. Siku moja Afisa mmoja wa Ubalozi wetu kule Roma akaamua kuandika kwa Travel Agency wote Italy kwamba kuanzia mwezi wa Kwanza tarehe moja ukitaka kwenda Zanzibar visa huipati kule, lazima uje Ubalozini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa watu Italy wanatoka miji mbalimbali; wengine wanatoka Nepals, wengine Frolence, wengine wapi; kwa hiyo, ukiwaambia kwamba walazimike kwenda Roma, maana yake utafanya usumbufu na kupunguza watalii Zanzibar. Sasa ilipokuja ile habari, wote sisi, Waziri wa Muungano ndio unaaambiwa, namtafuta Waziri wa Mambo ya Ndani ambaye anahusika na masuala ya Uhamiaji, kumwuliza, hana habari. Waziri wa Mambo ya Nje mwenye Ubalozi, hana habari, kwamba jambo kubwa kama hili limeamuliwa lakini hana habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbe ulikuwa ni uamuzi wa mtu mmoja. Sasa wenzetu Wazanzibari, baadhi walivyolipata wakajua tayari ni siasa hapa, tunaminywa, wanataka kutuua, wanataka kutumaliza, utalii ndiyo uchumi wetu, hawatupendi. Ikawa jambo kubwa! Kumbe kuuliza, hamna mtu yeyote mkubwa wa Serikali anayelijua. Ni Afisa mmoja tu. Kwa hiyo, tukalazimika kubadilisha ule uamuzi ili utaratibu ule wa zamani wa kupata visa on arrival uendelee pale pale; na unaendelea mpaka sasa hivi. Hatukutangaza kujitutumua kwamba tumesaidia, kwa sababu ni mambo ya kila siku ya kawaida ya utendaji wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, kuna kikao kikubwa kinakuja cha tarehe 28 mwezi wa Nne, baadhi ya mambo ambayo Waheshimiwa Mbunge wameyazungumza; mambo ya VAT na mifumo ya kodi yatazungumzwa na kumalizwa na Mawaziri wa Fedha pamoja na wataalam wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kombo amezungumza kwamba uchumi wa Zanzibar unakufa, uchumi unasimama, mfumo mbovu. Sasa nadhani tueleze, maana nimemsikiliza kwa makini sana na nilichokisikia ni lawama, nikawa na kalamu yangu nangoja aniambie nini sasa tufanye ili tuweze kufanikiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu usajili wa meli, ni jambo ambalo wote tunalijua na kuna hoja hapa kwamba Zanzibar sasa inanyang’anywa usajili wa meli. Bahati nzuri nimeshughulika nalo hili mwenyewe binafsi. Ambacho kinataka kufanywa ni kwamba zoezi la usajili wa meli liwe
shirikishi. Tufahamu kwamba hizi meli zinabeba bendera ya Tanzania ya nchi yetu. Wote tunajua meli kadhaa zimekamatwa na mihadarati, nyingine zinabeba silaha, nyingine zinatia nanga katika bandari zilizozuiwa, nyingine zinakiuka vikwazo vya Umoja wa Mataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania imeitwa na kuaibishwa mara nyingi kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, tumetishiwa kuwekewa vikwazo vya kiuchumi kama nchi. Wasiwasi wetu mkubwa ni kwamba hizi meli zimekutwa na silaha na mihadarati, Mungu epusha siku ingekutwa na watu (human trafficking) ndiyo ingekuwa shida kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wote tunajua kwamba Mamlaka ya Kusajili Meli za Nje ni mamlaka ya nchi, lakini huko nyuma kulikuwa na makubaliano kwamba Zanzibar itafanya kwa niaba ya Tanzania na itabaki na hayo mapato, kabisa. Hili ni jambo ambalo wengi hawajui. Iliamuliwa kwamba Zanzibar ifanye kwa niaba yetu wote na ibaki na mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukatokea utaratibu pale kwamba wamemtafuta Agent Dubai, ndio ana muhuri wa Tanzania. Fikiria nchi kubwa ya Tanzania, mtu pale Dubai ana kaofisi, ndio anawakabidhi watu bendera ya Tanzania. Hatumjui ni nani? Sasa kilichofanyika na bahati nzuri mimi nilishiriki, tumesema, sawa, sahihi iendelee kuwa ya Waziri wa Zanzibar, lakini vyombo vya usalama vishiriki, meli zinazoomba bendera ya Tanzania tuzijue zinatoka nchi gani? Zinataka kufanya shughuli gani ili tulinde sifa na heshima ya nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndugu yangu akija kusema hapa kwamba tumewanyang’anya na nini, nadhani hatutendei haki na anatulaumu bila haki kabisa kwa kweli. Tunachotaka kufanya ni jambo zuri kabisa ambalo siyo litaisaidia tu Serikali ya Jamhuri ya Muungano, hata Zanzibar yenyewe itaisaidia. Kwa sababu tungenyang’anywa huu usajili kama nchi kutokana na makosa ya hizo meli, hata Zanzibar haya mapato yasingekuwepo. Kwa hiyo, hili linafanyika kwa nia njema na kwa ajili ya manufaa ya watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Pondeza namshukuru kwa pongezi. Ni kweli kuna changamoto kwenye kiwango cha deni la umeme na wote tunajua masuala ya VAT, tunajua calculations zinazotokana na uwekezaji wa miundombinu na jambo hili bahati nzuri Wizara zinakaa na zinaendelea kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la usajili wa vyombo vya moto, bahati nzuri AG yupo hapa. Suala lile limeshughulikiwa muda mrefu. Sisi tunataka gari yoyote ikisajiliwa Zanzibar iwe sawa na imesajiliwa Bara na ikisajiliwa Bara iwe sawa na imesajiliwa Zanzibar. Nasi Ofisi ya Makamu wa Rais, jambo hili tulilisukuma sana na mimi binafsi kwa nguvu zangu zote na Mawaziri wahusika wanajua; na viongozi wetu Wakuu, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu wametuunga mkono. Tulifikisha jambo hilo mpaka kwenye vikao muhimu vya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri jambo hili lina dimensions za masuala ya kodi na hicho kipengele kimeenda kutazamwa. Imani yetu ni kwamba katika mabadiliko ya sheria mchanganyiko, miscellaneous amendment ni kwamba jambo hili litaingizwa ili tuweze kubadillisha hizi sheria ili magari yaruhusiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nami nakubaliana na Waheshimiwa Wabunge, ni aibu kwa gari ya Zambia kutembea kwa urahisi Tanzania kuliko gari ya Zanzibar. Hilo jambo hamna anayeona aibu kulisema, hata sisi tunaona ni aibu vilevile. Tutalirekebisha, kwa sababu Serikali imeonesha utayari na lilishaingia hadi kwenye vikao vikubwa vya Serikali na lilipitishwa huko nyuma muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vikao, tangu kwenye mchango wa hotuba ya Waziri Mkuu, Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanazungumza kwamba mnakaa vikao, kero haziishi. Labda Waheshimiwa Wajumbe watupe njia mbadala ya kuzungumza zaidi ya vikao, kwa sababu vikao ndiyo mahali pakubwa ambapo tunaweza kuzungumza na kufanya maamuzi na yakafuatiliwa utekelezaji wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu alizungumza katika kuhitimisha hotuba yake kwamba kikao kikubwa ni kile cha Kamati ya pamoja chini ya Mheshimiwa Makamu wa Rais na maamuzi ya kila kikao ni maamuzi ya kiserikali yenye nguvu ya kiserikali na sisi kazi yetu ni kuyafuatilia na kuhakikisha kwamba yanatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata mchango wa Mheshimiwa Machano na tunapokea mapendekezo na ushauri aliotupa kuhusu fursa za utalii na kwenye simu na kuhusu vyombo vya moto, nimelizungumzia. Malipo ya ujenzi wa Ofisi, hili limewekwa kwenye bajeti kwa sababu ni deni na litaendelea kulipwa. Ahadi za viongozi, tutazifuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema pale awali, kwamba yale ambayo hatujayazungumza, tutayajibu kwa maandishi; yapo mambo ya mifuko ya plastick kwenye masuala ya mazingira. Dhamira yetu ya kuzuia kabisa mifuko ya plastick ipo pale pale na tutalitekeleza hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mwisho kabisa kwa kusema kwamba mwaka 1965, mwaka mmoja baada ya kuwa na Muungano wetu, kulikuwa na Mkutano wa Pamoja wa TANU na ASP wa kupendekeza Mgombea Urais wa Muungano. Kwenye ule Mkutano Mheshimiwa Karume alimpendekeza Mwalimu Nyerere kuwa Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ule Mkutano, Mwalimu Nyerere aliuhadithia ule mkutano na hadithi hiyo aliirudia mara nyingi jinsi Muungano huu ulivyokuja. Aliwaambia Wajumbe na Mzee Karume akiwepo kwamba Shehe Karume, ninyi Wazanzibari mkiwa tayari kuungana, Wabara nasi tutakuwa tayari. Marehemu Mzee Karume akajibu, wewe unazungumzia utayari wa nini? Hii habari ya kuwa tayari ya nini? Sisi tuko tayari. Ita Waandishi wa Habari sasa hivi, tutangaze sisi ni nchi moja, wewe Rais. Mwalimu akasema, hapana, mambo haya yanahitaji sheria, na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nazungumza hili tujue kwamba urithi wa Muungano wetu chanzo chake ni nini? Dhamira ya Muungano wetu ilitokana na nini? Ilitokana na nyoyo, dira na maono ya viongozi wetu Wakuu, Waasisi wa Taifa hili kwamba tumetawaliwa na tukaleta mapinduzi na tukaleta Uhuru. Tunao uwezo kabisa wa kutengeneza mipaka mipya ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi Watanzania hatujui thamani tuliyonayo duniani kwamba ni nchi pekee iliyotengeneza mipaka mipya kama nchi, tunachukulia hili jambo la mzaha tu. Tumetengeneza mipaka mipya na Taifa jipya kwa utashi wetu. Sasa hii habari ya kwamba mkopo umechelewa, hiki kimechelewa, naomba sana tusiweke doa kwenye jambo hili kubwa katika changamoto ambazo kabisa tuna uwezo wa kuzimaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika kwamba mtu unaoitwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na unapata manufaa kutokana na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, halafu unakuja unaupaka masizi Muungano ambao wote sisi ni warithi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, imani yangu kwamba tutapitisha bajeti hii ili baada ya hapa tuendelee kufanya kazi kwa pamoja kuimarisha Muungano wetu, nchi yetu hii iendelee kupata sifa kubwa iliyonayo duniani. Kama nilivyosema asubuhi kwenye hotuba yetu ni kwamba sisi sote tutaondoka hapa duniani, lakini legacy yetu kubwa ni kuondoka Muungano huu ukiwa imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wote, wana CCM wenzangu ambao sote tunasema kwamba tunataka kumsaidia Mheshimiwa Rais, namna kubwa ya kumsaidia Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha kwamba anamaliza wakati wake Muungano huu ukiwepo na ukiwa imara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia bajeti hii na nianze kwa kukupongeza kwa jinsi unavyoongoza Bunge letu vizuri kwa busara na hekima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mpango, Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wa Fedha, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote. Nimefuatilia mijadala ya bajeti hata kabla ya hapo, mijadala mbalimbali iliyohusu Wizara ya Fedha. Bahati mbaya sana katika baadhi ya mambo niliyobaini ni mashambulizi binafsi kwa Mheshimiwa Dkt. Mpango (personal attack), kwamba kuna wakati tabia yake, kwamba ana kiburi, ilikuwa inazungumzwa kuna wakati hata elimu yake inatiliwa mashaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingi kilichopo mezani huwa ni hoja, lakini bahati mbaya, mimi bahati nzuri nimepata kumfahamu Mheshimiwa Dkt. Mpango miaka kumi tumekuwa wote, alikuwa msaidizi wa Rais, Uchumi mimi nilikuwa Msaidizi wa Rais, Hotuba, nimefanya nae kazi kwa karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kujua humility au humbleness ni Dkt. Mpango, hii habari ya kiburi, binafsi na wote ambao tuna-interact naye binafsi hiyo haipo. Kwa hiyo nadhani wakati mwingine humu ndani ya Bunge tupingane tu na ni haki na ni sahihi, kuwa na mawazo tofauti ya alicholeta mezani lakini tunapomwendea binafsi tunakuwa tunakosea. Wakati mwingine sio yeye tu hata humu ndani baina ya Wabunge na Wabunge, umebaini Mbunge anapotoa hoja kinachojibiwa sio alichosema bali ni yeye yukoje na anaishi wapi na anafanya shughuli gani na yote ambayo yamezungumzwa yanakuwa sio tena hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Bunge la namna hiyo nadhani sio Bunge unalolitaka na sio Bunge linalostahili hadhi na uzito wako kama wewe Spika. Kwa hiyo, nataka ni-vouch, nimtetee Dkt. Mpango kwamba namfahamu na pia ukiondoa tu tabia yake ya kusikiliza na kuheshimu kila mtu, pia ni msomi mzuri bila shaka yoyote. Amefanya kazi Benki ya Dunia, ameaminiwa na Marais wawili, amepitia kwenye mikono ya Profesa Ndulu ambaye tunamsifu ni gwiji wa uchumi hapa nchini, ameaminiwa nje ya nchi na ndani ya nchi na pia ni mcha Mungu, kaka yake ni Askofu anatoka huko katika familia ya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Dkt. Ashatu wote ambao tunapishana naye kwenye corridor hatuwezi kusema kwamba, ana kiburi, tunamjua kwamba mtu ana heshima. Vilevile watalaam wa Wizara ya Fedha wakiongozwa na Bwana Dotto na wao pia ukimfuata bwana Dotto anakusikiliza na anafanya maamuzi akielewa jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niliona wakati tunaongelea bajeti hawa viongozi wetu wakuu ambao tumewapa kazi kubwa sana ya kuandaa bajeti na kuiwasilisha na kujibu siyo kazi ndogo wanaifanya kwa niaba yetu sisi Watanzania. Hivyo, tusiwapeleke kule ambapo tutazidi kuwatia msongo wa mawazo kwamba kazi wanayofanya hatuithamini. Kwa hiyo, nawapongeza kwa weledi wao lakini pia kwa hulka zao.

Mheshimiwa Spika, naomba nikuthibitishie kwamba sikukaa chemba na Mheshimiwa Dkt. Mpango kabla ya kuzungumza hapa siku ya leo. Kwa hiyo hizi ni hisia kabisa binafsi na zinawasilisha mawazo mengi hapa katika Baraza la Mawaziri na Wabunge wengi ambao tunafanya kazi na Mheshimiwa Dkt. Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mambo kadhaa yamezungumzwa kuhusu muungano hasa kubwa ni hoja ya Mheshimiwa Dkt. Ally Yussuf Suleiman ambaye ametaja mambo matatu, ambayo napenda kuchukua nafasi hii kuyajibu harakaharaka.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ni akaunti ya pamoja, amesema muda mrefu akaunti hii haijaanzishwa. Ni kweli na akaunti hii ya pamoja imewekwa ni hitaji la kikatiba kifungu cha 133 cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kinaelekeza kwamba kuwe na Mfuko wa Akaunti ya Pamoja ya Fedha ambayo itakuwa sehemu ya Mfuko Mkuu wa Hazina ambapo kutawekwa fedha yote itakayochangwa na Serikali mbili kwa kiasi kitakachoaamuliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha. Hilo ndiyo neno la msingi, kwa kiasi kitakachoamuliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Akaunti hii ya Pamoja haijakuwepo kwa sababu mapendekezo ya Tume ya Pamoja ya Fedha kuhusu kiwango cha mgawanyo ndiyo yanafanyiwa kazi na Serikali sasa hivi. Hili ni jambo kubwa linahitaji uamuzi wa Mabaraza yote mawili ya Mawaziri ya pande zote mbili na linahitaji input kubwa ya wataalam.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kinachoendelea sasa hivi ni kusubiri maamuzi baada ya wataalam kuwa wanamalizia kazi yao. Kwa hiyo, sisi kama Serikali azma ya kutimiza matakwa ya kikatiba bado ipo palepale, lakini kwa kuwa ni jambo kubwa lazima tuliendee kwa umakini na utaratibu ili liweze kufanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, suala la pili lililozungumzwa kuhusu Muungano ni suala la mchakato wa sasa hivi unaoendelea wa usajili wa meli. Kama unavyofahamu Tanzania ina aina mbili ya usajili wa meli; kuna usajili wa meli za ndani na usajili wa meli za nje zinazopeperusha Bendera ya Tanzania. Kwamba mtu yuko nje ya Tanzania ana meli yake, lakini anataka atumie Bendera ya Tanzania. Usajili huo unafanywa na Mamlaka Zanzibar ndiyo tulivyokubaliana, usajili wa meli za ndani unafanywa na SUMATRA. Sasa kulitokea changamoto ya kutokuwepo na uangalifu na umakini katika usajili wa meli za nje zinazopeperusha Bendera ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kilichojitokeza ni kwamba meli zinazopeperusha Bendera za Tanzania zilikutwa nje ya nchi zinafanya makosa makubwa, kubeba silaha, magendo, madawa ya kulevya na kupaki kwenye Bandari zisizoruhusiwa. Kwa hiyo, Serikali ambacho tumeamua kufanya siyo kuinyang’anya Zanzibar mamlaka ya usajili hapana, kwamba hili jambo la usajili tushiriki wote. Kwamba asiwe mtu Dubai ana muhuri tu yeye anagonga tu na kukabidhi bendera, lazima vyombo vya Usalama vya nchi vishiriki, kwa sababu tunapotoa bendera yetu, ni alama ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tulikubaliana kwamba wenzetu watafanya lakini wasifanye peke yao kuwe na input ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama na due diligence wa meli zote zinazoomba kutumia Bendera ya Tanzania. Kwa hiyo, hicho ndicho kinachofanyika na wala wenzetu Wazanzibari wasione tunawapora na kwa kweli ni muhimu haya mambo kuyajua kabla ya kuyasema, kwa sababu yanaamsha hisia ambazo si sahihi.

Mheshimiwa Spika, la mwisho ni Kisiwa cha Fungu Mbaraka au Latham; kwamba Mheshimiwa Dkt. Ally Yussuf Suleiman alisema kwamba Tanzania Bara inataka kupora Kisiwa hiki kwa sababu kuna rasilimali. Labda niseme kwamba nchi yetu ni moja hatujafikia mahali pa kugombea eneo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kinaitwa Fungu Mbaraka au Latham kipo katikati hapa Bahari ya Hindi. Kwa hiyo, kuna dhana inajengeka kwamba kuna mgogoro kati ya Bara na Zanzibar kuhusu umiliki wa Kisiwa hicho.

Mheshimiwa Spika, chanzo cha mgogoro ni kwamba inawezekana eneo lile lina mafuta. Sasa hii dhana inaenea na inaamsha hisia. Sasa niseme tu kwamba huko nyuma wakati suala la mafuta ni la Muungano na TPDC ndiyo ilikuwa inatoa leseni ni kweli pale mahali palitolewa blocks za kuchimba, kutafuta mafuta.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya wale waliyotafuta mafuta hawakuyapata, kwa hiyo wakarudisha zile block, kwa hiyo, mpaka leo lile eneo halina mtu anayetafuta mafuta. Kwa hiyo dhana kwamba tunagombea eneo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania siyo sahihi, Katiba zetu ziko wazi kuhusu maeneo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nchi yetu hii ni moja, Zanzibar ikinufaika Tanzania imenufaika, Bara ikinufaika Tanzania imenufaika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba kwa wenzetu Wanzazibari na Watanzania kwa ujumla kusijengeke dhana kwamba tunagombana kuhusu eneo lolote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, umezungumza kuhusu lugha humu ndani za ukabila na ukanda na mengineyo. Hata hivyo, kuna moja ambalo ni muhimu kulizungumza lugha zinazohusu Muungano wetu. Namna ambavyo tunauchangia na kuuelezea Muungano wetu ni kana kwamba bado hatujakubaliana kuhusu umuhimu wake na kwamba tumeamua kuungana. Kuna lugha kali sana ambazo zinafadhaisha watu wa upande mmoja na kudhalilisha upande mmoja au mwingine.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningependa utumie rungu lako na kiti chako na joho lako na busara zako kukemea hizi lugha ambazo zina-condemn kwa ujumla watu wa upande mmoja au mwingine kuhusu Muungano. Muungano wetu sisi tumeamua kuwa nchi moja, tumeamua kuwa jeuri na kutengeneza mipaka yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, naomba urithi huo tuulinde na Bunge lako lichukue uongozi katika kuulinda urithi huo.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, naomba nishukuru kwa fursa uliyonipa ya kuja kuhitimisha hoja hii hapa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwashukuru wachangiaji wote, kwanza kwa Kamati zote mbili: Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Kamati ya Katiba na Sheria kwa taarifa nzuri walizozitoa pamoja na ushauri, maoni na mapendekezo ambayo wameyatoa katika taarifa zao. Pia napenda niwashukuru wachangiaji wote waliochangia kwa maandishi walikuwa 25, waliochangia kwa kuzungumza walikuwa 9, jumla watu 34.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuipongeza Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa taarifa yao waliyosoma na maneno yao walitueleza na yote tumeyapokea na yote ni ya kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimshukuru Naibu Waziri wa Fedha ambaye ametusaidia kuelezea baadhi ya mambo na kujibu baadhi ya hoja. Pia namshukuru Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mheshimiwa Mwalimu Sima naye kwa mchango wake na majibu aliyoyatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye masuala machache ya jumla ambayo Waheshimiwa Wabunge waliyachangia. Kwanza suala la biashara kati ya Zanzibar na Bara ni jambo ambalo limejitokeza katika michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi waliochangia masuala ya Muungano. Bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha ametusaidia kujibu kwamba changmoto za kikodi ndiyo zilizokuwa zinakwamisha biashara kati ya Bara na Zanzibar zilitokana na mfumo tofauti wa ukadiriaji wa kodi kwa bidhaa zinazoingia katika vituo vya forodha vilivyoko upande wa Zanzibar na vituo vya forodha vilivyoko upande wa Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hilo sasa linashughulikiwa kwa kuweka mfumo mmoja wa ukadiriaji wa kodi kiasi kwamba bidhaa itakayoingia kwenye kituo cha forodha cha Zanzibar ikadiriwe kodi sawa na kituo chochote ambacho bidhaa hiyo imeingia kwa upande wa Bara. Imani yetu ni kwamba hilo litapunguza malalamiko na maelezo kwamba kunakutozwa kodi mara mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua haja ya kushughulikia masuala ya fedha na biashara kwa wakati wote, Kamati ya Pamoja ya kushughulikia changamoto za masuala ya Muungano iliunda Kamati Ndogo ya Fedha, Biashara na Uchumi ya Mawaziri, Makatibu Wakuu na wataalam ambayo itakuwa inakutana mara mbili kwa mwaka kushughulikia masuala ya fedha, uchumi na biashara yanayojitokeza mara kwa mara. Imani yetu ni kwamba mfumo huu na Kamati hii sasa itasaidia kusukuma mambo haya kwa haraka zaidi na kutatua changamoto za biashara zinazojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yetu sisi tuliopo katika Ofisi ya Makamu wa Rais ni kwamba uchumi wa Tanzania Bara ni mkubwa kuliko uchumi wa Zanzibar na Zanzibar lazima ifikie soko la Bara na Bara vilevile lazima iwe na uwezo wa kufikia soko la Zanzibar bila vikwazo vyovyote. Muungano huu ni wa kisiasa, kijamii pia kiuchumi. Kwa hiyo, imani yetu ni kwamba moja ya shabaha za Muungano ni kuleta ustawi wa watu wa pande zote na Muungano usionekane kikwazo cha ustawi wa upande mmoja au mwingine. Sisi katika Ofisi ya Makamu wa Rais, kwa maelekezo ya Mheshimiwa Makamu wa Rais ni kwamba tufanye jithada zote ili fursa za uchumi, biashara na ustawi na zenyewe ziendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Bara na Zanzibar wamekuwa wanafanya biashara hata kabla ya Muungano kwa miaka mingi, hata kabla ya Uhuru, hata kabla ya Mapinduzi. Imani yetu ni kwamba kuwepo kwa Serikali kusiwe kikwazo kwa biashara ya asili ambayo imekuwepo kwa miaka mingi kati ya watu wa pande zote mbili. Hiyo ni dhamira yetu kwamba ukubwa wa soko la Bara usaidie kujenga uchumi wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Tume ya Pamoja ya Fedha, nadhani Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha amelijibu lakini nitapenda niongezee machache. Ni kweli Tume ya Pamoja ya Fedha imeundwa kwa mujibu wa Katiba na vilevile Mfuko wa Pamoja na wenyewe umeundwa kwa mujibu wa Katiba. Hili suala linajirudia mara kwa mara hapa Bungeni kuhusu lini Mfuko huo utaanzishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakumbuka kwamba kwa mujibu wa Katiba, moja ya kazi za Tume ya Pamoja ya Fedha ni kuchunguza kwa wakati wote mfumo wa shughuli za fedha wa Jamhuri ya Muungano na pia uhusiano katika mambo ya kifedha kati ya Serikali mbili. Hiyo ni moja ya majukumu matatu ya Tume ya Pamoja. Tume hiyo ilifanya kazi kubwa sana kuanzia miaka ya 90 na mwaka 2006 ikawasilisha ripoti Serikalini, nakumbuka ilikuwa tarehe 9 Oktoba, 2006 kwa Waziri wa Fedha wakati huo Mama Zakia Meghji na ripoti ile Tume ilikuwa ni ya mapendekezo ya vigezo vya kuchangia na kugawana mapato ya Muungano. Ni ripoti iliyotokana na study ya muda mrefu kwenye nchi nyingi kuhusu mfumo sahihi, bora na na sawia (equitable) wa kugawana mapato na kuchangia mapato ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya ripoti ile kupokelewa, Serikali zote mbili ziliahidi kuifanyia kazi na kweli baada ya pale ikapelekwa kwenye Baraza la Mawaziri wataalam wakaifanyia kazi, Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mara kadhaa mapendekezo yale yalitengeneza cabinet paper ili yaweze kupitishwa na tuwe na mfumo bora ikiwemo kuanzisha Akaunti ya Pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya hilo halikutokea kwa sababu moja au nyingine hadi tukaanza mchakato wa Katiba ambapo ndiyo ulionekana kwamba utakuwa mfumo bora zaidi wa kushughulikia jambo hili. Kwa hiyo, imani yetu ni kwamba mchakato wa Katiba utakaendelea basi suala hili pia litaendelea kushughulikiwa. Tunashukuru kwamba pia Wizara ya Fedha inaendelea kulishughulikia suala hili. Kwa hiyo, Akaunti ya Pamoja ni takwa la Kikatiba na lazima litekelezwe na lazima litatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vikao vya Kamati ya Pamoja, tumesikia kwenye taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani ikisema kwamba vikao hivi havina maana yoyote kwamba vinakaa, hatuoni matunda na hakuna utekelezaji na kadhalika. Labda niseme tu kwamba mwaka 2006 tulipoanzisha utaratibu mpya wa Kamati ya Pamoja ya Fedha kulikuwa na changamoto 15 za Muungano na kwa kutumia mfumo huu wa vikao zimetatuliwa changamoto 11 zimebaki changamoto tano (5).

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hizi zimetatuliwa katika vikao na siyo kwa njia nyingine na siku zote mambo yote yanamalizwa kupitia vikao. Kwa hiyo, sisi hatuamini kabisa kwamba vikao hivi havina maana kwa sababu tumeona matunda yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu wanapokuwa na mambo wanayamaliza kupitia vikao. Kwa hiyo, ingependeza kama wenzetu Waheshimiwa wangetueleza zaidi ya vikao ni ipi namna bora zaidi ya kuzungumza mambo ya Muungano. Sisi tunaamini vikao ni namna bora zaidi. Bahati nzuri katika kikao cha tarehe 9 Februari, 2019, hapa Dodoma cha Kamati ya Pamoja tuliamua kurasimisha na kuimarisha mfumo wa vikao hivi ili tuweze kufuatilia maelekezo na maagizo yake na kuhakikisha kwamba yanayoamuliwa yanatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa kwamba vikao vinakaa na changamoto za Muungano haziiishi. Naomba niseme hapa kwamba changamoto za Muungano hazitakuja kuisha hata siku moja na dhana kwamba kwa sababu kuna changamoto basi Muungano haufai ni potofu kabisa. Siku ya kwanza Muungano umepitishwa, siku ya pili kulitokea changamoto ya namna ya kuunganisha majeshi, mfumo wa fedha na masuala ya ushirikiano wa kimataifa na mambo mengine, siku ya pili tu ya Muungano. Nakumbuka wakati ule tulikubaliana kwamba masuala ya fedha yatakuwa ya pamoja lakini kukawa na mkanganyiko kuhusu nafasi ya Peoples Bank of Zanzibar na BoT lakini mambo haya yalimalizwa kwa vikao na leo changamoto ile hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miaka ya 55 ya Muungano changamoto ambazo leo hatuzizungumzii kwa sababu zimemalizwa ni nyingi. Kwa hiyo, sisi tunaamini kwamba Muungano huu kikubwa ni mfumo na utaratibu ambao tutauweka wa kumaliza changamoto na hilo ndio ambalo tunalifanya sasa. Kudhani kwamba hakutakuwa na changamoto ni ndoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeongelewa kuhusu mainstreaming ya masuala ya Muungano, utaona ni hoja iliyotolewa na Mheshimiwa Saada Mkuya. Sisi tunadhani kwamba ni hoja muhimu na ya msingi. Wewe unafahamu na Waheshimiwa Wabunge wanafahamu kwamba kwenye kila bajeti ya kila Wizara iwe ni ya Maji, Miundombinu au Maliasili kuna mambo huwa hayakosi UKIMWI na rushwa siku zote hata kama hayahusu sekta hizo lakini yamo kwenye bajeti zote za Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunaamini kwamba tufike mahali kwamba kwenye kila bajeti ya kila Wizara iwe ya Muungano isiwe na Muungano basi suala la Muungano na lenyewe liwepo kama ripoti ambayo inatolewa. Hili tunalizungumza Serikalini kwa sababu kwa Wizara za Muungano kuna ulazima wa kushirikiana na mambo ya kutekeleza lakini kwenye Wizara ambazo siyo za Muungano tunahamasisha ushirikiano. Kwa hiyo, itapendeza hapa kwenye hotuba za bajeti kila Wizara ikasema imeshirikiana vipi na upande wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda na wenzetu wa Zanzibar kama tutazungumza na kukubaliana pia katika bajeti zao na wenyewe waseme katika mwaka uliopita wa fedha kama ambavyo kwenye masuala ya rushwa na UKIMWI wanaripoti basi vilevile kwenye masuala ya Muungano kuwa na ripoti. Tunaamini hatua hii itasaidia kuimarisha Muungano na italazimisha wenzetu na wengine waripoti kuhusu masuala ya muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme tu kwamba watu wengi hawajui lakini hakuna Wizara isiyo ya Muungano kwenye Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, iwe ni Wizara ya Maji ambayo siyo jambo la Muungano au Wizara ya Utalii ambayo siyo jambo la Muungano, Wizara zote ni za Muungano. Mheshimiwa Dkt. Kibwangalla anaitwa Waziri wa Maliasili na Utalii wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu hakuna Wizara ya Bara, Wizara zote ni za Muungano. Kwa hiyo, kila Wizara ina wajibu wa kuchukua hatua za kuhakikisha kwamba angalau tunashirikiana na upande wa pili kuhusu masuala ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imetoka hapa hoja kwamba Serikali ya CCM haina nia na Muungano huu. Mimi huwa sipendi kuingia kwenye mambo ya kushambuliana kwenye vyama na mambo ya siasa za aina hiyo, lakini kauli hii lazima ijibiwe. Katika mambo ambayo yanapaswa kuwa nje ya siasa ni masuala ya Muungano. Kwenye nchi zote kuna baadhi ya mambo ambayo siasa haipaswi kuingizwa. Kwenye nchi za wenzetu kuna mambo ambayo yamemalizwa siyo tena mjadala na kwenye nchi yetu mimi imani yangu ni kwamba Muungano ni jambo ambalo tunapaswa kuwa tumelimaza halipaswi kuwa na u-CCM, u-CUF, u-ACT wala namna nyingine yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano wa nchi ya Marekani, wao ni Muungano wa Kifederali na ule Muungano uliletwa kwa vita, kuna nchi zilikuwa hazitaki kuwa sehemu ya Muungano na vita ikapiganwa na wale ambao hawakutaka kuwa sehemu ya Muungano wakaingizwa kwenye Muungano kwa kushindwa kwenye vita hasa Majimbo ya Kusini. Tangu wakati ule leo United States of America, aidha, iwepo au isiwepo siyo tena hoja ya siasa wala kampeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani tunapaswa kufika hapo kwamba wakati wa uchaguzi haipaswi Muungano wetu kuwa kwenye referendum. Kwa sababu kilichopo sasa hivi ni kila uchaguzi unapofanyika Muungano ni kama vile upo kwenye kura ya maoni. Kwa hiyo, kama nchi tunapaswa kuondoka huko. Wenzetu ambao wameungana kila mahali, hata Marekani Muungano wao una miaka zaidi ya 200, lakini kila siku wana kauli yao wanasema, to strive for a more perfect union. Kwamba, Muungano wao wa miaka 200 bado hauko perfect. kwa hiyo, nasi leo tukija hapa Bungeni tukataka leo miaka 55 tuwe na a perfect union tutakuwa tunaomba mambo ambayo hayako tayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Muungano huu kazi yetu ni kuendelea kuujenga na namna ya kuujenga siyo kuusimanga na kuchukulia changamoto ndogo na kuupaka matope na kuupa jina baya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia zaidi ya 94 ya Watanzania wamezaliwa ndani ya Muungano, hawajui Tanganyika, wanajua wamezaliwa ndani ya Muungano na hawana pengine pa kwenda na utambulisho wao ni wa Muungano. Kwa hiyo, nawaomba na kuwasihi Waheshimiwa Wabunge ambao huwa tunarushiana vijembe na maneno na wale wanasiasa ambao wanatumaini changamoto za Muungano zitasaidia kuwabeba, basi tuache hivyo, wote tufanye kazi pamoja kuuimarisha Muungano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi Rasmi ya Upinzani imezungumzia kuhusu muundo wa Muungano na kwamba ndiyo chanzo cha changamoto na kwamba haufai na ndiyo umetuletea matatizo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa kwenda kwenye mjadala huu kwa sababu ni mrefu na wote tunajua mjadala huu tuliufanya wakati tunafanya mchakato wa Katiba. Ambacho naweza kusema ni kwamba, Waasisi wa Muungano, Mwalimu Nyerere na Mzee Karume, kabla hawajaamua Muungano wa aina tuliyonayo leo, walitafakari miundo yote ya kila aina, wakatazama dunia nzima, wakatazama mazingira yetu, wakatazama haiba ya watu wetu, wakatazama ukubwa wa pande zote mbili na wakaamua kuwa na Muungano wa kipekee duniani ambao ndiyo tulionao leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiniuliza mimi sababu ya kudumu kwa Muungano huu, tofauti na Muungano wa Senegal na Gambia, tofauti na Muungano wa Misri, Syria na kwingineko ni kwa sababu ya muundo wake. Tunatofautiana; wengine wanadhani Muungano wetu una shida kwa sababu ya muundo wake, lakini sisi tunaamini Muungano wetu umedumu kwa sababu ya muundo wake. Kwa hiyo, kikubwa ni kuendelea kuimarisha mifumo na taratibu za kushughulikia masuala yanayojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuna bahati kwamba Muungano wetu una bahati ya kuundwa katika misingi ya kijamii, kwa sababu mahusiano ya kijamii ya watu wa pande zote yamekuwepo kabla ya mapinduzi, yamekuwepo kabla ya uhuru na yamekuwepo kabla ya Muungano. Kikubwa tu ni sisi kuendelea kuimarisha masuala ya kitaasisi na kisheria na kiutaratibu ili tuendelee kuwatendea haki watu ambao ni ndugu wa pande zote mbili za Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumziwa hapa suala la vyombo vya moto, kwamba haipendezi ikawa kuna ugumu wa kuingia na gari lako kutoka upande wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana kabisa kwamba ni jambo linalokera, linaloudhi kwamba gari kutoka Zambia au Malawi, linavinjari kwa urahisi katika nchi yetu, lakini gari kutoka Zanzibar linapata bughudha. Hilo jambo halikubaliki kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri sasa Serikali imeanza kulishughulikia jambo hilo na Mwanasheria Mkuu wa Serikalin anafahamu kwamba kulikuwa tayari na mapendekezo ya mabadiliko ya Sheria ya Usajili wa Magari na Sheria nadhani ya Polisi na ilishafika kwenye Mkutano wa Kamati ya Baraza la Mawaziri ya Katiba na Bunge ili mabadiliko yafanyike kuhakikisha kwamba jambo hilo linakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya tukashauriwa kwamba ili utaratibu huo udumu na uwe imara, tuhakikishe kwamba zinawekwa taratibu ili wale watu ambao wanaweza kutumia mwanya kuingiza magari na badaye kuyauza kwa upande mwingine, basi wasifanikiwe. Sasa study hiyo iliyofanywa na TRA na wengine imekamilika, nasi tunaamini kwamba wachache ambao wanaweza kutumia fursa hiyo vibaya wasiwaharibie watu wengi wema ambao wanataka kusafiri na vyombo vyao vya moto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utaratibu huo utawekwa na ni imani yangu kwamba mabadiliko hayo ya sheria yatafywa mapema kupitia kwa wenzetu ili jambo hilo tulimalize. Ni kero kubwa na ni aibu kusema kweli. Kwa hiyo, imani yetu ni kwamba litakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la mifuko ya plastic. Naomba niseme, tumezungumza kwa kirefu kwenye hotuba yetu, lakini naomba niseme tu kwamba dhamira hii ni njema. Kwenye hili tumejipanga vizuri kwa sababu tumeshirikisha wadau mapema zaidi. Tunaamini kwamba suala hili ili tufanikiwe ni lazima twende hatua kwa hatua. Kwa sasa hatuwezi kupiga marufuku kila kitu; kuna baadhi ya vifungashio vinavyotumia plastick ambavyo ni lazima vitumie plastick, kwa mfano, mikate, maziwa, madawa na vinginevyo. Imani yetu ni kwamba, kwa sasa vitaruhusiwa ili tusilete bughudha na mtikisiko kwenye uchumi na kuongeza bei za bidhaa kwa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaanza na mifuko hii ambayo ni kero, hata hivyo kwa vifungashio tutaweka standards ili viweze kukusanywa na kurejelezwa. Hiyo, tunaamini tutafanikiwa. Hata wale wenye chupa za plastick vile vile imani na mpango wetu ni kuweka ulazima wa wao kushiriki kwenye mipango ya recycling, kwamba huwezi kuwa unazalisha chupa za Kilimanjaro halafu huna habari hiyo chupa inaishia wapi? Lazima ushiriki kwenye utaratibu wa kuirejesha na kuirejeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kanuni mpya pia zitatoa mahitaji hayo. Naomba Waheshimiwa Wabunge tusaidiane, kwa sababu tutakapofanikiwa jambo hili tutakuwa tumefanya jambo la kihistoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shaka kuhusu mbadala kwamba, je, mbadala upo na unatosha? Naomba niwaambie kwamba wenzetu Wakenya ambao wamepiga marufuku mifuko ya plastic, mifuko yao ya karatasi wanaitoa Tanzania. Wenzetu Warwanda, ukienda kule Mufindi Paper Mills, malighafi yote ya mifuko ya karatasi ya Rwanda inatoka Mufindi na Rwanda inasifika, Kigali, kama mji safi kabisa hapa Afrika, sababu ni nini? Sababu ni sisi ndio tunawapa karatasi, wanapata mifuko ya karatasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wale wametuhakikishia kwamba uwezo wa ku-supply mifuko ya karatasi hapa nchini wanao na kwamba, changamoto yetu kubwa kwa sasa ni kuhakikisha wanaongeza production na usambazaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni tunazotoa zitatoa adhabu kwa wanaouza mifuko, wanaoweka na kwa wanaoingiza ndani ya nchi. Kunaweza kukatokea mtikisiko na malalamiko kidogo kwenye zoezi hili, naomba Waheshimiwa Wabunge muiunge mkono Serikali kuhakikisha kwamba, jambo hili linafanikiwa. Kwa sababu, siku zote hakuwezi kukosa malalamiko kwenye masuala makubwa ya mabadiliko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matumizi ya mkaa na ukataji wa miti, hii ni changamoto kubwa sana sana. Kila dadika moja inayoenda hapa nchini, misitu inayofyekwa ni sawa na kiwanja cha mpira. Tangu niongee hapa nadhani ni dakika 15, misitu iliyofyekwa ni sawa na viwanja vya mipira
15. Tena hizi ni takwimu za chini na sehemu kubwa ni ukataji wa mkaa, kilimo kisicho endelevu, uzururaji wa mifugo, na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wataalam wa mazingira hapa, akina Mheshimiwa Dkt. Sware wanafahamu kwamba misitu ina thamani katika mifumo ya kiikolojia na utajiri wa nchi unapimwa kwenye mambo mengi; kuna utajiri wa watu wenyewe, utajiri wa vitu na utajiri wa maliasili. Katika nchi zinazoongoza duniani kwa utajiri wa maliasili, wanaita Natural Resources Wealth Per Capita. Tanzania ni moja kati ya nchi zinazoongoza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miaka 20 iliyopita utajiri wa Tanzania kwa maliasili kwa maana thamani ya mito, maziwa, misitu, na kadhalika, thamani yake per capita inashuka kwa asilimia 35 kwa miaka 20 iliyopita, ingawa GDP per capita inapanda, lakini natural resources per capita inashuka chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dalili pekee ya kwamba maendeleo siyo sustainable ni pale utajiri wenu wa maliasili unaposhuka wakati utajiri mwingine unaenda juu. Kuna wakati hata ule unaenda utashuka utakutana na ule wa chini. Kwa hiyo, tuna wajibu mkubwa kuhakikisha kwamba maendeleo tunayoyatafuta ili yawe endelevu, hatuna budi kulinda maliasili zetu kwa nguvu zetu zote kwa sababu, ndiyo utajiri tulionao. Kwa hiyo, sisi ndani ya Serikali tunazungumza na wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Wizara nyingine husika ili kuwa na makubaliano kuhusu mwenendo wa kulinda rasilimali za nchi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, hili jambo tunazungumza na wenzetu kwamba sisi tunaamini msitu uliosimama na miti iliyosimama ina thamani hata kwenye kilimo kwa sababu hata mahindi ili yazae lazima kuwe na wale wadudu na nyuki wanaofanya polination nao wanatoka kwenye misitu. Ukipewa shamba sasa hivi lenye msitu, usipokata msitu unanyang’anywa kwa sababu hujaliendeleza, ehee! Nasi tunaamini kwamba msitu vilevile unaposimama na wenyewe una thamani yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili tunalizungumza kwamba kuna mwenzetu mmoja akiona mti umesimama anauona ni gogo na lenyewe ni chanzo cha mapato. Kwa upande mwingine ule mti pia unaweza kuuweka nyuki na kuzalisha. Kwa hiyo, ni mambo ambayo tunazungumza ndani ya Serikali ili kuhakikisha kwamba tunatunza nchi yetu; na maelekezo ya viongozi wetu, mmemsikia Mheshimiwa Rais alipokuwa Njombe alisema tulinde misitu yetu kwa nguvu zetu zote na mapori yetu yote. Imani yangu ni kwamba tutaendelea kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tumewasikia kilio chenu kuhusu kasi ya ukataji wa miti na kasi ya nchi yetu kuwa jangwa. Ukombozi haupo kwenye kupanda miti, ukombozi upo kwenye kutunza miti iliyopo isikatwe, kwa sababu miti iliyopandwa haifiki asilimia nane ya miti yote iliyopo nchini. Tusipokata miti ni bora zaidi kuliko kuhangaika kupanda miti mingine. Kwa hiyo, huko ndiyo ambako jitihada zitaelekezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa kuhusu utendaji wa NEMC na nilizungumza asubuhi kuhusu reforms ambazo tunafanya. Tumepokea kabisa malalamiko kuhusu utendaji wa NEMC na malalamiko hayo ni ya kweli kwa sababu, kulikuwa na changamoto kubwa za ucheleweshaji wa vibali, gharama za vibali na mambo mengineyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza kwa kirefu asubuhi hatua tunazochukua. Bahati nzuri tumepata uongozi mzuri, tunaye Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC ambaye tuko naye hapa, Profesa Asnath Chagu, tuna Mkurugenzi Mkuu mpya, anapanga safu yake vizuri. Tumesikia changamoto ya watumishi wachache wa NEMC, bahati nzuri wenzetu wa Utumishi wametusaidia, wametupa kibali cha kuajiri watu 30 mwaka huu, lakini zaidi ya hapo tumewaelekeza watu wa NEMC kwamba, kuna vijana wengi sana wamesoma mazingira na jiografia kwenye vyuo vikuu na hawana kazi na ni vijana wazuri na wasomi. Tumesema kwa sababu kazi za NEMC ni nyingi, wawachukue kwa mkataba kama interns na kuwatumia kwenye kazi za kwenda kufuatilia, kusimamia, na kadhalika, wapate posho na uzoefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa hivi tunao 40 na miezi michache tutaongeza 100 na mwaka ujao tutaongeza 100 wengine kuhakikisha kwamba footprints ya NEMC nchi nzima inakuwa kubwa. Tunafungua Ofisi za Kanda ili kuhaklikisha kwamba NEMC inatoa huduma kote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, NEMC sasa hivi inabadilisha mtazamo wake kutoka taasisi ya kipolisi na kuwa taasisi ya huduma zaidi kwa wawekezaji na kwa wananchi. Nimewaambia watu wa NEMC, nyie mkionekana mnafunga viwanda, mnatoza fine, mnakusanya pesa, sawa ni kazi zenu, lakini ukisoma sheria mna kazi kubwa na muhimu zaidi ikiwemo utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sheria inasema NEMC inapaswa kuweka orodha ya milima na vilima vyote nchini. Sheria ilisema, ndani ya miaka mitano baada ya sheria kuundwa kuwe na orodha iliyochapishwa kwenye Gazeti la Serikali kuhusu milima na vilima vyote nchini na hatari ya mazingira kwa vilima hivyo. Hiyo ni kazi ya NEMC. NEMC inaruhusiwa kumiliki maeneo yaliyolindwa kwa Sheria ya Mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutabadilisha mwelekeo wa NEMC ionekane ni taasisi kubwa na yenye heshima na yenye hadhi, siyo ya kufukuzana na watu na kuchelewesha vibali, na kadhalika. Kwa hiyo, mtaiona NEMC tofauti na tutaendelea kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niseme kwamba, tunataka uwekezaji na uwekezaji ni muhimu, lakini tunaamini uwekezaji lazima uende sambamba na hifadhi ya mazingira. Sasa nataka kusema, mtu yeyote ambaye anacheleweshewa kibali na NEMC au anaamini NEMC inamcheleweshea kibali, aje kwetu sisi moja kwa moja tutamsaidia papo hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho limezungumzwa suala la UNHCR Kigoma na madhara ya wakimbizi kwenye uharibifu wa mazingira. Tumeongea na wenzetu wa Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Wakimbizi kuhakikisha kwamba kwanza makambi yetu yanafanyiwa Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA) na hali ya mazingira inarejeshwa na kwamba wananchi pia wanapata manufaa na huduma ambazo wakimbizi wanazipata ikiwemo maji, na kadhalika. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma hili tunalishughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la mfumo mzima wa usimamizi wa mazingira. Sheria ya mazingira imetengeneza architecture, mfumo wa usimamizi wa mazingira. Sheria ya Mazingira imetoa maelekezo kwa Wizara na Taasisi nyingine za Umma na binafsi, lakini hususan na Serikali za Mitaa kuhusu mambo ya kufanya. Kwa hiyo, Maafisa wa Mazingira wanaajiriwa na Halmashauri na kamati zinapaswa kuundwa kwenye ngazi ya Halmashauri. Kwa hiyo, kikubwa tunachofanya sisi ni kushirikiana na TAMISEMI kuhakikisha kwamba ule mfumo wa usimamizi wa mazingira ambao unahusu Wizara zote unasimamiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Mazingira inasema kila Wizara iwe na mratibu wa mazingira na kila Halmashauri iwe na Afisa Mazingira na kila Sekretarieti ya Mkoa iwe na Mratibu wa Mazingira. Kila kijiji kiwe na Kamati ya Mazingira, kila Kitongoji, kila Mtaa, kila Kata, kila Wilaya. Hapo ndipo mfumo mzima wa usimamizi wa mazingira utakuwa umekamilika na kwamba NEMC peke yake haiwezi kuwa kwenye kila Mtaa, kila Kijiji na kila Kitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa tumeifanya katika mwaka uliopita kuhakikisha kwamba mfumo huu unakuwepo, kuna baadhi ya mikoa imefanya kazi nzuri sana ya kuhakikisha kwamba Mitaa yote, Vijiji vyote vina Kamati ya Mazingira na matunda tunayaona katika usimamizi wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala limezungumzwa la kutotosha fedha. Labda niseme tu kwamba fedha siku zote hazitoshi na hasa kwenye nchi kama yetu. Sasa ambacho nataka kusema ni kwamba kuna Bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais ya Mazingira, pia kuna fedha za mazingira zinazokuja nchini katika ujumla wake. Ukiangalia Bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais na ukaichukulia kwamba ndiyo fedha za mazingira hapa nchini utakuwa umefanya makosa. Nitatoa mfano kwamba, sisi Ofisi ya Makamu wa Rais tumewatafutia Wizara ya Maji fedha kwenye Mfuko wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Tabia-Nchi (Green Climate Fund). Tumehakikisha wamezipata. Fedha zile ni shilingi bilioni 250 ambazo zinaenda kuleta maji Simiyu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa zingekuwa kwenye bajeti yetu, si ajabu kusingekuwa na maneno. Kuna fedha zimepitia kwetu lakini ziko Wizara ya Kilimo; kuna fedha zimepitia kwetu, lakini ziko Wizara ya Mifugo. Kwa hiyo, inawezekana fedha zikaonekana hapa kidogo, sisi kazi yetu wakati mwingine ni kuwatafutia wengine fedha kupitia mikataba ya Kimataifa ambayo sisi ni wanachama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutaendelea kufanya hivyo. Tunaamini kwamba ni kweli rasilimali zinahitajika zaidi na tunaamini pale Mfuko wa Mazingira utakapokuwa umeanza kazi, basi na wenyewe utachangia katika kuhakikisha kwamba fedha zaidi zinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala mengine yamezungumziwa ya GMO, Mheshimiwa Chiza; masuala ya matumizi ya maji kwenye umwagiliaji, masuala ya matumizi ya gesi na Mheshimiwa Ruth Mollel, ameongea kuhusu suala la nafuu ya kodi kwenye mitungi ya gesi ili kuokoa misitu. Hilo tutazungumza na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba linafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho ni kikubwa na cha msingi ni kwamba tunaona na tunafarijika sana na kupanuka kwa nishati mbadala ya mkaa. Kiwango cha gesi ya mitungi kinachotumika mwaka huu ni kikubwa mara mbili ya kilichotumika mwaka jana 2018 na tunaamini kadiri miaka inavyoenda na tunaona uwekezaji katika eneo hilo, imani yetu ni kwamba tutafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mita 60 nilizungumzia asubuhi kwamba tunaweka kanuni na utaratibu wa kuweza kuhakikisha kwamba tunafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani mambo yale makubwa na ya msingi, suala la elimu ya Muungano ni kweli lazima nikiri kwamba hatujafanya vizuri, wakati mwingine tunafanya mambo makubwa lakini hatuyazungumzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja kwamba vikao vya Muungano ni vya siri kwamba hakuna transparency, hiyo siyo kweli. Udhaifu wetu ni kwamba labda baada ya kikao tulipaswa kuitisha press conference ili watu wajue. Kwa hiyo, tumechukua maoni na ushauri kuhusu namna ya kuelezea wananchi kuhusu nini kinafanyika na ofisi zetu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa nirudi tena kwenye suala la Muungano kwa kifupi kwamba, kuna kazi nyingi sana kwenye Muungano zinafanyika hasa kupitia kwa viongozi wakubwa, hasa kupitia kwa wataalam, miradi, uhusiano na ushirikiano uliopo lakini mjadala wetu kuhusu Muungano umejikita kwenye changamoto. Sisi tunadhani kwamba tunayo kazi ya kuonyesha kwamba definition ya Muungano sio vikao vya changamoto bali ni mambo mengine mengi yanayofanyika ambayo hayaonekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nitoe ahadi kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba wale ambao hoja zao sijazigusa na hata wale ambao nimezigusa basi tutaziandika vizuri, tutatoa majibu vizuri na tutawapatia kabla Bunge la bajeti hii halijakwisha ili waweze kusoma majibu yao kwa sababu muda wa kujibu hapa wakati mwingine hautoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.

MWENYEKITI: Toa hoja.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima na taadhima kubwa, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Fedha na Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, napenda nianze kwa kukupongeza kwa uongozi wako mahiri wa Bunge letu kama ulivyojidhihirisha pia hivi karibuni ulipotuongoza kwenda Misri pamoja na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha pamoja na timu nzima ya Wakurugenzi, Kamishna wa Bajeti na wengineo kwa kuandaa bajeti hii ya Serikali ambayo imesomwa vizuri na Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Spika, yamezungumziwa masuala mbalimbali ya Muungano katika michango hii na mimi nitapenda kujikita katika mambo kadhaa. Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika kujibu hoja atajibu mahsusi kuhusu miradi iliyotajwa na iliyochangiwa na Wabunge ambayo walipenda kupata maelezo, mradi wa Bandari ya Mpigaduri, jengo la uwanja wa ndege, barabara ya Chake na miradi mingineyo, Mheshimiwa Waziri wa Fedha anayo maelezo mazuri na atayatoa. Mimi niongee kwa ujumla tu kuhusu masuala ya Muungano na hasa namna tulivyouzungumzia Muungano humu ndani ya Bunge letu.

Mheshimiwa Spika, wewe unafahamu kwamba Tanzania na sisi sote tuliomo ni nyumba na ni nyumba ya urithi kwa kweli kwetu sisi sote kwa sababu imejengwa na watu wengine na sisi tumeirithi, tunaishi katika Tanzania iliyojengwa na watu wengine na viongozi wetu walioijenga wametangulia mbele ya haki. Namna tulivyouzungumzia Muungano katika michango hii kwa baadhi ya Wabunge maneno yanajenga lakini maneno pia yanabomoa. Baadhi ya maneno yaliyotumika, baadhi ya lugha zilizotumika hazichangii kujenga nyumba yetu hii tuliyoirithi kwa viongozi wetu waliotangulia mbele za haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya maneno humu yametuhumu, yametusi na kwa kweli yameleta fadhaa kubwa. Mimi naomba kwa heshima ya Bunge lako, nchi yetu na kwa dhana nzima ya kuimarisha umoja, mshikamano na upendo miongoni mwetu, baadhi ya maneno kwa kweli ifike mahali yasiruhusiwe kutumika ndani ya Bunge lako Tukufu hasa maneno ambayo yanachangia kuweka ufa katika Muungano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nilipata bahati ya kwenda kuhudhuria bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakati inasomwa siku ya Alhamisi wiki iliyopita na niliisikia bajeti imesomwa na Waziri Balozi Ramia. Baadhi ya mchango humu ndani katika bajeti yetu hii kuu ya Serikali ya Muungano imenukuu kwamba bajeti iliyosomwa Zanzibar ilirejea na kuzungumza na kwamba Waziri Mpango na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina roho mbaya, haina nia njema kwa Zanzibar ina hasada, wivu, chuki na kwamba Waziri Mpango na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamegoma kufanya masuala ambayo yataleta maendeleo kwa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwepo kwenye bajeti ile, hayo maneno yaliyonukuliwa kwamba yamezungumzwa na Waziri wa Fedha wa Zanzibar hayakunukuliwa hivyo, siyo sahihi. Bajeti ile ilisomwa kwa staha, kwa ustaarabu na ilieleza mipango ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Mimi napenda nimpongeze Waziri wa Fedha wa Zanzibar pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuandaa na kusoma bajeti nzuri na ya kujasiri ambayo ina nia ya kuleta maendeleo ya Zanzibar. Kwa hiyo, tusiwatie maneno midomoni viongozi wa Zanzibar na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kusukuma ajenda zetu za kuleta mgawanyiko katika Muungano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kama nchi tumeweka utaratibu wa kushughulikia masuala ya Muungano, yanapojitokeza tunayazungumza na tunayafanyia kazi. Napenda niseme kwa taarifa kwamba kuna ndugu yangu kutoka Pemba alizungumza jana nadhani Mheshimiwa Mohamed Amour na sisi tunaotoka Tanga watu wa Pemba tuko karibu nao, ni ndugu zetu kwa sababu unapanda mashua tu unavuka, unafika Pemba. Ndugu yangu alitumia lugha ngumu kidogo kumsema Waziri Mpango na kuwasema viongozi wa Serikali na kukisema Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, ilichukua uvumilivu kwa baadhi yetu kutohamaki na ilikuwa inazungumzwa ni barabara kwamba kuna barabara ya kilometa 20, kilometa 40 imechelewa kujengwa kwa hiyo basi kwa sababu hiyo watu wote huku wana chuki, wivu, hasada. Kuna masuala mengi sana ya maendeleo ya Zanzibar, yanapojitokeza na mchango wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unapohitajika kuna utaratibu mzuri uliowekwa ambao unatumika katika kuyawasilisha na kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, mimi nilipata bahati ya kuwa Msaidizi wa Rais Kikwete, mwaka 2005 – 2006 kulikuwa na changamoto ya umeme Pemba, kulikuwa na shida kubwa likaletwa kama suala kwamba Pemba kuna shida kubwa ya umeme katika utaratibu tuliouweka hayakutumika matusi, kejeli wala kudhalilishana. Lilivyochukuliwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikatafuta msaada Norway dola milioni 88 ukawekwa waya chini ya bahari kutoka Tanga kwenda Pemba kupeleka umeme. Huo ni msaada ambao Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliutafuta. Umeme ukapatikana Pemba bila matusi, kejeli au kudhalilishana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya katika miaka ya hivi karibuni ule umeme umeleta changamoto. Mimi ni kiongozi ninayetoka Tanga, watu wenye viwanda Tanga walikuja kutulalamikia mbona Tanga mnasema tujenge viwanda lakini umeme hautoshi? Tukaenda kuwauliza TANESCO jamani mbona umeme Tanga hautoshi? Wakasema, jamani eeh mtuwie radhi, tumewapelekea wenzetu Pemba line moja ya umeme kwa sababu kuna tatizo. Hilo limefanyika bila matusi, kejeli au kudhalilishana. Kwa hiyo, Serikali hizi zinafanya kazi pamoja vizuri, zinashirikiana, hakuna haja ya kuja hapa Bungeni na kusema watu wana chuki, hasada, wanafiki na kadhalika. Maneno hayo yanabomoa nyumba yetu hii ya Tanzania ambayo sisi tumeirithi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa suala la Sheria ya Mikopo kwamba mabadiliko yameleta changamoto. Naomba niwataarifu Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, wiki iliyopita suala hilo imelileta rasmi kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na limeingizwa katika utaratibu wetu wa kawaida wa kushughulikia masuala ya Muungano. Hapa Bungeni siyo kwamba ndiyo linaletwa kwa mara ya kwanza na Wabunge, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenyewe imelileta na tayari Serikali zote mbili zinalifanyia kazi na litatolewa taarifa kuhusu namna linavyoshughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais na Rais Shein kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kipindi hiki cha miaka mitatu kuimarisha Muungano wetu. Mimi nakuomba na nakusihi sana Mzee wangu unayenipenda, naomba utusaidie Bunge lako lisiwe chanzo cha kuweka ufa katika Muungano wetu wacha watu wengine huko barabarani wafanye lakini siyo Wabunge, tena wakiwa ndani katika nyumba hii Tukufu na kula kiapo cha kuilinda Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utakumbuka mwaka 1992 ndani ya Bunge lilijitokeza kundi la Wabunge 55 ambao walitaka kuchukua hatua ambayo ingesababisha kuvunjika kwa Muungano wetu (G55), wakasema kuwepo na Serikali ya Tanganyika jambo ambalo kwa hakika lingesababisha kuvunjika kwa Muungano. Mwalimu Nyerere muasisi wa Muungano na baba wa Taifa letu aliingilia na akakaa na Wabunge pamoja na Wajumbe wa NEC, sisi tunafundishwa kwamba ni mara chache Mwalimu Nyerere ametoa chozi hadharani ni pale alipopokea mwili wa Sokoine, alipokuwa anamuelezea Mheshimiwa Kawawa na alipokuwa anataka Muungano huu udumu kwa kuwazuia wale watu 55 wasichukue hatua waliyokuwa wanataka kuichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusingependa kauli hizi zinazotoka humu zikataka kuleta hisia kama zile za mwaka 1992. Tunaomba utuongoze, ninyi ndiyo wazee mliobaki, mwalimu hayupo. Baadhi ya kauli zinazotoka humu zitafanya miili ya waasisi wetu ndani ya makaburi yao ianze kuzunguka kutokana na maneno yanayotoka ya kutaka kuivunja nchi yetu. Tunaomba sana utuongoze, uhodari wa kuwasema wengine ili kupata mtaji wa kisiasa, uhodari wa kuunajisi Muungano kwa maneno machafu ili kupata umaarufu wa kisiasa usikubalike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni jambo ambalo linakubalika kabisa kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina bajeti yake, ina Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na kuna Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa upande wa Zanzibar. Tunafahamu kabisa kwamba vyote hivyo vinahitaji rasilimali ili kutekelezwa na tunafahamu kabisa kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzana inayo nafasi katika kuhakikisha kwamba Zanzibar inapata uhakika wa rasilimali hizo. Hilo linafahamika na viongozi wetu wanalifahamu na wanalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimalize kwa kusema kwamba tumechagua viongozi mahiri kwa pande zote; Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Zanzibar, tuwaamini kwamba dhamira yao ni kufanya yote yanayopaswa kufanyika kuimarisha Muungano wetu. Tusishindane kwenye uhodari wa kuusema Muungano kama namna ya kuulinda. Tuwachie viongozi wetu na sisi kwa kauli zetu na kwa matendo yetu tuwasaidie katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inabaki moja ili kizazi hiki kiirithishe nchi yetu kwa kizazi kijacho bado ikiwa inaitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa nazungumza kwa mara ya kwanza tangu nipate heshima ya kushika nafasi hii, napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniamini katika nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakushukuru wewe kwa uongozi na ushauri wako katika kipindi hiki cha siku takribani 58 ambazo nimekuwa katika nafasi hii. Nakushukuru sana na naishukuru Kamati yako vile vile kwa miongozo mbalimbali na ushauri mbalimbali ambao umefanya mpaka tumeweza kufika hapa siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge kadhaa wamechangia katika Mpango kuhusu mambo yanayohusu sekta ya nishati. Kabla sijajibu, naomba nimpongeze Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na timu yake kwa kazi nzuri ya maandalizi ya Mpango ambao ni mzuri, unaotoa dira, pamoja na uwasilishaji na michango mizuri iliyotoka kwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo matatu ambayo ningependa kuyazungumzia ambayo yalichangiwa na Wabunge kwenye Wizara yetu. La kwanza kubwa ni suala REA. Tunaelewa kwamba usambazaji umeme vijijini ni jambo kubwa, ni jambo ambalo linagusa maisha ya Watanzania wengi, karibu Wabunge wote wana hoja na maswali kuhusu umeme katika maeneo yao. Sisi katika Serikali tunatambua umuhimu wa jambo hilo, sasa tumejipanga upya kuhusu utaratibu bora zaidi; wa kwanza, kuwapa taarfia Waheshimiwa Wabunge kuhusu miradi iliyopo katika maeneo yao; pili, kutengeneza na kutafuta rasilimali kwa maeneo ambayo bado hayajapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na changamoto kubwa sana ya takwimu ikiwemo classification ya wapi ni kijijini? Wapi siyo kijijini? Kwa hiyo, changamoto imetusabaishia tuwe na namba tofauti kuhusu idadi ya vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambacho tumeamua na kwa ridhaa yako, naomba rasmi kwamba katika Bunge la mwezi wa Pili, tutawaita Wakandarasi wote hapa Bungeni, tutakuwa na maonesho ya siku tatu kule nyuma, kila Mkandarasi wa kila Mkoa atakuwa na meza; na sisi wote tutahamia hapa ikiwemo ofisi nzima ya REA pamoja na Wizara; tutafanya semina kuhusu suala hili na kuhusu mpango wetu mpya.

Waheshimiwa Wabunge maswali yao yote yatajibiwa hapo hapo kuhusu kule ambako umeme haujaenda, umechelewa, unasuasua na unatarajiwa kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuanaamini kwamba tukilifanya hili jambo kwa wakati mmoja, hata tukikaa hapa wiki nzima kujibu maswali, kero na maoni na ushauri wa Wabunge kuhusu program hii mpya ambayo tunakuja nayo, basi itasaidia kama namna bora zaidi ya kubadilishana taarifa kati yetu sisi na Wabunge, lakini pia itatusaidia zaidi katika kukusanya takwimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi atunafahamu kwamba umeme hautumiki na Kijiji, umeme unaatumika na watu. Kwa hiyo, takwimu za kijiji ni nzuri zinatupa milestone kwamba tume-cover maeneo ya kiasi fulani; lakini mtu ambaye hajapata umeme nyumbani kwake na haujamfikia, takwimu kwamba umefika kijijini kwake, siyo takwimu ya maana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaelewa na mwelekeo mpya ni kupima nyumba zinazohitaji umeme na ambazo hazijapata umeme. Huko ndiko tunakokuja. Tunafahamu kwamba tuna idadi ya vitongoji hapa nchi 64,000; vitongoji vilivyopata umeme ni 27,000 tu na vitongoji zaidi ya 37,000 na kadhaa huko havijapata umeme. Kwa hiyo, tunakuja na mradi mkubwa zaidi ambao bahati nzuri wenzetu huko nyuma walishaanza nao kuuzungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba mahitaji ya rasilimali ni makubwa, ili vitongoji vyote 37,000 vipate umeme, tunahutaji shilingi trilioni 8. Tunafahamu kwamba haziwezi kupatikana kwa wakati mmoja, lakini support ya Bunge hili ni muhimu sana ili tuweze kupeleka umeme kila mahali.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, naomba atukutane mwezi wa Pili, tutakuwa na semina na maonesho ya muda mrefu. Kila Mbunge atajibuwa maswali yake yote kuhusu umeme katika maeneo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine lililozungumziwa ni kuunganisha mikoa iliyobaki kwa gridi. Plans zipo, mipango ipo na tumeielezea; Mkoa wa Rukwa, Kigoma, maeneo ya Mkoa wa Kagera pamoja na Mkoa wa Katavi. Tunaamini kwamba mpaka mwaka 2024 mikoa yote itakuwa imeunganishwa kwenye gridi ya Taifa kwa miradi tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa la mwisho nizungumze hili kubwa lililozungumzwa na Mheshimiwa Ester Bulaya la mradi wa Julius Nyerere. Sasa sisi tulipata barua ya tarehe 3 Septemba,kutoka Ofisi ya Bunge kwamba, Kamati ingependa kupata taarifa ya tulipofikia. Tulileta taarifa hiyo ipo kwenye mtandao wa Wajumbe wa Kamati na naamini Mheshimiwa Bulaya amepata taarifa hizo huko. Kwa hiyo, ni kweli kwamba, Serikali ya Awamu ya Sita ilipoingia madarakani iliupokea mradi huu ukiwa umechelewa kwa siku 477.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu tumefikia wapi kwa kila kipengele cha mradi kwa asilimia, hazina maana sana kwa sababu zinabadilika kila siku. Hata siku ya leo kuna kazi inafanyika, maana yeke ni kwamba, nikikupa asilimia leo, wiki ijayo zitakuwa ziko tofauti. Ni kweli mradi una changamoto ambazo alipokuja Mheshimiwa Makamu wa Rais kuutembelea alizieleza na sisi tulipokutana na Kamati ya Bunge pia tulizieleza. Ni changamoto za kawaida kwenye utekelezaji wa miradi mikubwa ya namna hii. Changamoto hizi hazifanyi mradi huu uonekane hauna maana. Changamoto hizi haziwezi kuturudisha nyuma wala kutuondoa katika nia ya kuutekeleza mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naambiwa kuna airport kubwa kule Ujerumani imechelewa miaka, akataja miradi mikubwa ya kimkakati katika nchi zilizoendelea ambayo imechelewa. Kuchelewa kwa mradi ni jambo la kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali tumechukua hatua pale ambapo kulikuwa na uzembe hatua zimechukuliwa kwa upande wa TANESCO na Wizarani, hizo ni changamoto za upande wetu. Kwa upande wa mkandarasi, mkataba baina yetu na mkandarasi unayo tiba kuhusu changamoto za ucheleweshaji na sisi tunafuata tiba hiyo. Tumeanza vikao na mkandarasi kuhusu namna ya kumaliza changamoto zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme tu kwamba, mazungumzo yanaendelea kati yetu na mkandarasi ambayo yana misingi minne. Kwanza ni kupunguza hizi siku za ucheleweshaji kutoka 477 zilizopo sasa na kujaribu kuona kama tunaweza tuka-squeeze tukaharakisha baadhi ya maeneo zikawa chache zaidi. Msingi wa pili, ni kuzuia kusiwe na ucheleweshaji zaidi. Msingi wa tatu, kazi ifanyike kwa ubora na viwango vinavyotarajiwa na msingi wa nne, kusiwe na ongezeko la gharama kwa upande wa Serikali. Kwa hiyo, mazungumzo yetu na mkandarasi yako katika misingi hiyo minne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nirudie kwamba, kauli aliyotoa Mheshimiwa Rais hapa Bungeni kwamba, miradi yote hii mikubwa ya kimkakati lazima itakamilika na lazima itatekelezwa. Naomba kuchelewa kwa mradi kwa siku 477, naomba nirudie kusionekane kwamba, ni tatizo litakalouua mradi huu. Sisi tumejipanga vizuri sana kuhakikisha kwamba, tunautekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe ambayo inazungumzwa sana ni tarehe inayokaribia ya kujaza maji kwenye bwawa. Kwa sababu, ilizungumzwa hapa Bungeni na nimeona clip inazungumza, ngoja nilitolee ufafanuzi kwamba, ilisemekana kwamba, tarehe 15 Novemba, basi maji yataanza kujazwa kwenye bwawa lile. Si ajabu kwa kadiri siku hii inavyokaribia itakuwa ni habari kubwa ambayo inaweza kutumika kuuchafua mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, tarehe hiyo itapita kabla hatujajaza maji na sababu ni mbili. Ili ujaze maji kwenye bwawa lazima masharti mawili yatimie; lazima uwe umejenga tuta kuu ambalo ni main dam, ule ukuta mkuu wa kuzuia maji kwa mita 95 juu ya usawa wa bahari, lile tuta linapaswa kuwa na mita 190 juu ya usawa wa bahari. Sasa ili uanze kujaza maji lazima uwe umefikia mita 95. Mpaka leo bahati nzuri tumeshapita mita hizo 95 juu ya usawa wa bahari kwa hiyo, sharti la kwanza la kujaza maji tumelifikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sharti la pili, ni kwamba, wakati tunajenga hili tuta kuu tulijenga njia ya kuchepusha mto pembeni, ili tupate nafasi ya kujenga. Sasa ili sasa ujaze maji lazima uzibe lile handaki ulilolijenga kuchepusha mto. Sasa ili uzibe lile handaki unahitajika milango mikubwa na vyuma takribani 14 na kila kimoja kina tani 26, ni machuma makubwa ya kuzuia lile handaki ili mto usiendelee kuchepuka wakati unajaza bwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ile milango imefika, lakini inahitaji crane kuibeba na kuziba, ile crane lazima itoke nje na crane hiyo haijafika bado. Kwa hiyo, tumetimiza sharti la kwanza la kujaza maji, lakini sharti la pili la kutuwezesha kuziba ule mchepusho hatujalifikia. Kwa hiyo, kwa hali na mwenendo hatutaweza kujaza maji kwenye bwawa kabla ya mwezi wa Machi. Tutawapa tarehe mahususi ya kuweza kuanza kwa kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya nikiamini kwamba, sisi ni viongozi katika Bunge hili, mradi huu ni wakwetu, ni mradi wa kimkakati, kufanikiwa kwa mradi huu ni kufanikiwa kwa nchi. Kicheko au kejeli yoyote kwa kuchelewa kwa mradi huu haimsaidii mtu yeyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekwishatokea kwamba, katika project management yoyote na katika miradi mikubwa haya mambo hutokea. Kwa hiyo, imani yangu ni kwamba, sisi tutashirikiana na tutaomba ushirikiano wa Bunge lako kuhakikisha kwamba, malengo yaliyowekwa ya mradi huu yanatimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kulizungumzia hili. Sasa hatuko hapa kumlaumu mtu, kazi hii tumepewa sisi ambao tumeteuliwa na tutaifanya kwa nguvu, uwezo na maarifa yetu yote kuhakikisha kwamba unakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho la LNG; naomba niwahakikishie Watanzania kwamba, mradi huu mkubwa kabisa wa kimkakati wa jumla ya shilingi trilioni 70, jana tumetengeneza historia kwa kuanza mazungumzo na makampuni ya mafuta na gesi. Kwa hiyo, nchi yetu itaenda kupata manufaa makubwa sana katika miaka ijayo kwa kuvuna gesi yetu kwa matumizi ya kuuza nje, lakini pia kwa ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, ndugu zangu wa Lindi na Kusini na Watanzania wote, tutapata nafasi ya kueleza fursa zitakazopatikana wakati wa utekelezaji na pia tutakuwa wawazi kuhusu mfumo wa mapato yatakayotokana na gesi hii na jinsi ambavyo nchi yetu na uchumi wetu utafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisitumie muda mrefu. Nafahamu yako mengi, tutayazungumza kwa kadri siku zinavyokuja ikiwemo mabadiliko ya mfumo wa uuzaji na ununuzi wa mafuta nchini ili kuweza kutoa nafuu kwa watumiaji wa dizeli na petroli na mafuta ya taa nchini, hatua ambazo nadhani mmeanza kuziona. Mengi na mazuri yatakuja katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa na nianze kwa kutoa pongezi kubwa kwa Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuandaa Mpango madhubuti waliouwasilisha hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana tulienda kwenye uchaguzi na kila chama kilitoa ahadi kwa Watanzania. Watanzania wakakiamini Chama cha Mapinduzi na wakaamini kwamba ahadi za CCM ndizo zinazotekelezeka, jukumu la kwanza kabisa la chama kinachoshinda uchaguzi ni kuunda Serikali. Kwa hiyo, Serikali imeundwa, Serikali imara na Serikali madhubuti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu la kwanza la Serikali iliyoundwa baada ya uchaguzi ni kutengeneza mpango unaotafsiri Ilani na ahadi za chama kilichoshinda. Hilo ndilo tunalolifanya sasa. Jukumu la pili la Serikali iliyoshinda ni kutengeneza bajeti za kila mwaka za kutekeleza mpango ambao tumesema unatafsiri ilani na ahadi za chama, hilo ndilo linalokuja katika kikao hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mantiki ya kawaida inasema kwamba kama wenzenu wameshinda, wameunda Serikali, wametengeneza mpango ambao unatafsiri yale yaliyowafanya washinde, wenzenu mnapaswa kuwapa nafasi watekeleze mipango yao na bajeti yao. Wanaposhindwa baada ya miaka mitano au katikati tunapofanya tathmini ndipo tunapokuja na kusema ninyi mmeshindwa. Hatuwezi wakati tunatengeneza mpango wetu ambao unatafsiri yale tuliyowaahidi Watanzania tunasimama tunasema ninyi kile, ninyi kile, ninyi hiki. Tupeni nafasi, ni Serikali mpya, tutekeleze ya kwetu katika mwaka wa kwanza kabisa wa Serikali hii ndipo tuje tuzungumze yale ambayo...
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa staili na kasi ya Serikali hii ya Awamu ya Tano hakuna hata chembe ya shaka kabisa kwamba yale tuliyoyaahidi, tuliyoyaandika katika Mpango wetu huu na katika bajeti tutakayoileta yatatekelezwa kwa ukamilifu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukitazama sura, kauli, umakini wa Rais wetu na Wajumbe wa Baraza lake la Mawaziri na Wabunge wa upande wa CCM kwa ujumla, hakuna shaka yoyote kwamba tumedhamiria kutengeneza nchi mpya. Tumedhamiria kutengeneza Taifa jipya, Taifa lenye haki, Taifa lenye usawa na Taifa lenye heshima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma katika miaka mingi tulijaribu kutengeneza Taifa la namna hiyo…
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Naibu Spika Taarifa!..
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshimia na taadhima napenda kuikataa taarifa hiyo na napenda kuikataa bila kueleza sababu, sababu za kuikataa ni dhahiri kabisa. Isingependeza kupoteza muda kueleza sababu za kuikataa kwa sababu zinaeleweka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika naomba niendelee …
NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naomba basi tusikilizane!
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa aina ya taarifa iliyotolewa haistahili hata kuielezea kwa nini naikataa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kwa kueleza kuhusu mazingira. Nashukuru sana kwamba katika Bunge hili kuna Wabunge wengi wanamazingira na naomba sana tutakapoleta bajeti yetu ya Ofisi ya Makamu wa Rais tutatoa dira mpya na mwelekeo mpya wa namna ya kulinda na kuhifadhi mazingira ya nchi yetu, tunaomba mtuunge mkono. Tutaeleza namna tunavyotaka kujenga uwezo wa kitaasisi wa Serikali na uwezo wa kifedha wa Serikali katika kugharamia shughuli za ulinzi wa mazingira. (Makofi)
Mwisho ni kuhusu Muungano, kuhusu Uchaguzi wa Zanzibar. Vitabu vinavyotuongoza kuhusu suala la Zanzibar kwa maana ya Katiba ya Zanzibar na Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar vinatuelekeza kwamba jambo hili limekwisha. Suala hili limekwisha, treni imeshaondoka kwenye kituo, wenzetu hawakushiriki, wamefanya uamuzi wa kimkakati ambao umewaondoa katika ushiriki wa siasa na maendeleo ya Zanzibar. Ni uamuzi wao, ni uamuzi ambao wataendelea kuujutia.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama CCM tunaamini kwamba ujenzi wa Taifa letu kwa ujumla ni jukumu letu sote na tunawakaribisha wenzetu hata kama wako nje ya Serikali kuendelea kushirikiana na sisi kuijenga Zanzibar na kuijenga Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza Viongozi Makatibu Wakuu wa Wizara na Watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara, ikiwemo TANROADs kwa kazi nzuri mnayoifanya. Kazi inaonekana na jitihada pia zinaonekana. Kwa miaka zaidi ya 20 sasa wananchi wa Kongowe na Bumbuli wamekuwa wanangoja barabara ya kwanza ya lami katika eneo hilo. Wamekuwa wanaipigia kura CCM kwa matumaini hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ahadi ya barabara ya kutoka Soni – Bumbuli – Kwashemshi – Korogwe kujengwa kwa kiwango cha lami bado imebaki ahadi ya kwenye Ilani na kwenye Kauli za Viongozi. Wananchi hawa sasa wanakata tamaa. Mwaka jana kwenye vitabu vya bajeti barabara hii ilionesha sifuri, yaani haikupangiwa fedha. Jambo hili lilitusikitisha. Mwaka huu tumeona fedha kidogo sana kwa ajili ya kumalizia design kwa kipande cha mwisho. Naomba na kupendekeza kwamba, kwa kuwa kipande cha Soni – Bumbuli tayari design imefanyika, fedha zipangwe kuanza angalau kilomita 10 za lami mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za kupandishwa madaraja kuwa za TANROADs; vilevile tulipendekeza barabara mbili na kuzipitisha katika michakato yote husika kwa ajili ya kupandishwa madaraja. Barabara hizo ni: Kwanza, barabara ya Soni - Baga – Ngwashi – Milingano – Mashawa na pili ni Soni – Mponda – Tawota – Keronge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi zinaunganisha Wilaya na Majimbo matatu. Tunasubiri majibu ya Wizara kwa maombi haya.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja iliyopo mezani ya Kamati ya Nishati na Madini. Yako masuala mengi mengine tutayajibu kwa maandishi na sitaweza kuyafikia yote lakini nitachangia kwenye masuala mawili matatu. La kwanza ni bei ya mafuta ambayo nadhani wote tunafahamu mwenendo wa bei ya mafuta duniani, ukitazama ile shepu ya curve ya bei kuanzia mwaka 2014 ambapo bei ya sasa ya mafuta iko juu kama iliyokuwa 2014. Kwa hiyo, unapata bakuli kwamba 2014 ilikuwa inashuka halafu inashuka ikaanza kupanda mwaka 2021 mpaka sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna dhana kwamba Mheshimiwa Rais ameingia mama Samia bei ya mafuta imepanda kila kitu kimepanda lakini kazi kubwa imefanyika, ya kuondoa tozo mbalimbali kuhakikisha kwamba wananchi wanapata nafuu ya bei ya mafuta. Sasa bei ya mafuta asilimia zaidi ya 50 inachangiwa na bei ya mafuta duniani asilimia 39 ni kodi na tozo mbalimbali hapa nchini. Kwa hiyo, yale mengineyo ya miundombinu ni kama asilimia 10 asilimia 11 ukitazama, ukiondoa tu kodi zile za TRA mapato ambayo yapo Ring-fenced kwenye mafuta ni shilingi 513. Tuna shilingi 263 ya Mfuko wa Barabara tuna shilingi 100 ya TARURA, tuna shilingi 100 ya REA, tuna shilingi tano ya maji jumla ni shilingi 513. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiamua kuzitoa zote hizo mafuta tunaweza kununua kwa shilingi 1,800/=, lakini tunanunua shilingi 3,000, shilingi 2,300 kwa sababu kuna hizo na zile kodi nyingine. Kwa hiyo, kupanga ni kuchagua tunataka bei ya chini ya mafuta maana yake either tuondoe kwenye maji, tuondoe kwenye REA, tuondoe kwenye TARURA au tuondoe kwenye Mfuko wa Barabara. Sasa, huo ndio uhalisia Serikali imechukua na itaendelea kuchukua hatua mbalimbali, za kupunguza makali kwenye bei na tumefanya tumetoa fedha nyingi. Kwa sababu, kama sio hatua za Serikali leo bei ya mafuta watu wangekuwa, wananunua hata shilingi 2,600 lakini tumezishusha kupunguza makali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kufanya hivyo lakini mazingira ya dunia mnayajua moja ya nchi kubwa zinazozalisha mafuta kwa wingi Duniani, ni Urusi na sasa hivi kuna shamrashamra ya vita kule na leo pipa limeenda dola 90 na kama vita ikitokea itafika dola 100. Kwa hiyo, ni vizuri tukawaeleza wananchi uhalisia kwa sababu tunaweza tukaja hapa, tukasema Serikali haijafanya kitu kupunguza ifanye zaidi lakini uhalisia ndio huo. Tutaendelea kuchukua hatua bila shaka na siajabu tukachukua maamuzi magumu kuhakikisha kwamba, bei kubwa ya mafuta haiathiri shughuli za uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Suala la miundombinu limezungumzwa kwamba miaka yote limekuwa linazungumzwa na halifanyiwi kazi ni kweli. Kuna meli hapa zinakuja zinachukua siku mpaka 19 hazijashusha nyingine mpaka zinaondoka na sio tu za mafuta ,hata meli nyingine zinakaa pale kwenye outer and carriage mpaka siku za kwenda mahali pengine zinaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niwape habari njema kwamba kabla ya mwisho wa mwezi huu tutasaini IMU na makampuni makubwa mawili ya kuweza kufumua miundombinu yote ya uingizaji/ushusha na uingizaji wa mafuta. Tunakwenda kuibadilisha TIPPER na kuweka uwekezaji mkubwa ambao utaongeza uwezo mara tatu kwa TIPPER. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi meli ikija ya mafuta ya dizeli inashusha kwenye kituo kinaitwa SPM ambalo bomba lake ni jembamba kwa hiyo, meli ina pressure kubwa bomba jembamba na hatuwezi kufuta kushusha mafuta Dar es Salaam mpaka twende Tanga ambapo bandari ni ndogo. Kwa hiyo, tumeamua tutaweka mabomba makubwa zaidi na sio dizeli peke yake tutaboresha matanki na tutabadilisha. Hiyo kazi itachukua kama miaka mitatu lakini itabadilisha kabisa mfumo mzima wa ushushaji wa mafuta hapa nchini. Hilo ni jambo liko tayari tumelifanyia kazi katika kipindi cha miezi hii michache iliyopita kwa siku zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kilio kile kwamba miaka yote linazungumzwa halifanyiki basi safari hii, linafanyika sawasawa kutokana na uongozi wa Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, nilizungumza ya mafuta amezungumza vizuri sana Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya hapa kwa siku sekta yetu ya mafuta sisi inachangia shilingi bilioni 5.1 kwenye shughuli za maendeleo. Kwa mwaka shilingi 1.8 trillion ni sekta ambayo ni very sensitive ni sekta ambayo lazima tuilee na kuikuza vizuri sasa la mafuta hilo limeisha hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni la kukatikakatika kwa umeme limezungumzwa sana na niseme tu kwamba na Wabunge baadhi wamezungumza vizuri sana hapa na lina dimensions nyingi; na nimesikia Mbunge hapa mmoja akisema watu mnatudanganya na nini. Hakuna mtu kwenye Wizara/TANESCO anapenda umeme ukatike na hakuna mtu anafanya makusudi kukata umeme in fact, watu wetu wa TANESCO sasa hivi hata saa 8 usiku ukipiga simu mahali umeme umekatika wako field wanajaribu kurudisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyopo ni changamoto ya legacy ya muda mrefu kimataifa inabidi utenge asilimia 10 mpaka asilimia 12 ya pato ghafi la kampuni (utility) kwa ajili ya (R&M) Repair and Maintenance. TANESCO mwaka jana imepata mapato ya 1.8 trillion shillings maana yake Repair and Maintenance ilipaswa kuwa shilingi bilioni 180 mwaka juzi imepata Shilingi 1.7 trillion, Repair and Maintenance ilipaswa kuwa shilingi bilioni 170 na hivyo na hivyo na hivyo. Sasa uliza ngapi zimetengwa for the past ten years sasa hauwezi, kutotenga na hao walioweka hizi standards ni wanasayansi na kote duniani wanafanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa utakuja utalaumu Waziri kaja umeme unakatika lakini we have to do the necessary things ili turekebishe. Hapa nataka niwaambie kuna line za ugavi za usambazaji wa umeme ambazo nyingi ni 33KV na 11KV, ndio 33KV unasambaza umeme mitaani na standard ni kilomita 100 kwa 33KV umeme. Sasa kuna line inatoka Dodoma inakwenda Kongwa inakwenda Mpwapwa inakwenda Gairo inakwenda Kiteto ya 33KV kilomita 1,600 wakati inapaswa kufanya kilomita 100. Kuna line ya 11KV inapaswa kupeleka umeme kule Chanika kilomita 30 lakini inapeleka umeme 206.

Mheshimiwa Mwenyekiti, line inakwenda Lindi kutoka Mkuranga pale ni ya kusambaza umeme mitaani 33KV sasa umeme Lindi unategemea utakuwaje, watu wanajenga wanaanzisha biashara wanaanzisha viwanda lazima kutakuwa unstable na hii yote amezungumza Mheshimiwa Gulamali kule Igunga ni nchi nzima. Sasa, sisi tumeyakuta hayo lazima tufanye kwa hiyo tume-design mradi mkubwa wa dollar bilioni 1.9 wa ku-upgrade sub-stations na hizi lines zote ambazo zinazungumzwa kuhakikisha kwamba umeme kwenye gridi upo stable. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wabunge mtu- support sub-stations kwa mfano, nchi nzima kuna distribution sub-stations 67 tu wakati kimuundo TANESCO ina Wilaya 132 lakini una sub-stations 67 na kati ya hizo 39 ziko Dar es Salaam sasa unategemea stability ya umeme itapatikana vipi wakati, hauna sub-stations nchini na katika hiyo sub-stations uliza ambazo zimechakaa ni majority. Tumetafuta fedha tumetenga kwanza ku-refurbish sub-stations 19 na kujenga nyingine mpya 59. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeyakuta matatizo na tunayashughulikia kwa uhakika hapa juzi kulikuwa na habari ya mgao umekwenda umetokea kutokana na kule visimani tumesimamisha kufanya mgao pale Ubungo kwa Mheshimiwa hapa kaka yangu. Zile wire za sub-stations zile ziko wazi haziko insulated ukitokea upepo zikigusana tu Ubungo sub-station inachomoka. Ikichomoka Ubungo sub-station half of Dar es Salaam haina umeme na kingine ni kuzivalisha tu juzi tumefanya hiyo kazi nchi nzima tumezivalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vikombe vina-cracks ikinyesha mvua vina-conduct umeme unakatika. Sasa hatutaki kusema haya maneno sana sisi tunaomba mtupe muda Mheshimiwa Waziri aliyepita kaka yangu Kalemani alikuwa na miaka minne kwenye … (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri nitakuongezea dakika tatu ili uweze kuhitimisha hoja yako.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante alikuwa na miaka minne kwenye nafasi hii na amefanya kazi nzuri mimi nina miezi minne tuombe uhai, nina imani na Rais na mimi nipate miaka minne halafu tuone kama tutakuja kuzungumza haya mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais aliyepita marehemu mpendwa wetu alikuwa na miaka sita kwenye nafasi hii mama Samia ana mwaka mmoja na yeye, tuombe uhai apate miaka sita halafu tuone kama tutakuja kuzungumza matatizo kama haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuvumiliane tupeane muda maneno ya kushambuliana binafsi yanasikitisha kwamba Waziri kapanda helicopter kaweka hivi na nini hii sio sifa ya Mbunge. Hatuko hapa kutupiana mawe hii ni meli yetu wote nikifeli mimi imefeli nchi akifeli Rais imefeli nchi. Kama una matatizo ya Mheshimiwa Samia Suluhu kuwa Rais au mimi kuwa Waziri tutafute jambo lingine sio mambo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni Julius Nyerere nimebakia dakika mbili katika ulizonipa. Julius Nyerere nilivyoripoti kwenye ofisi hii status ya kwanza kuomba ni ya mradi kwa wataalam nao wakanipa taarifa kwamba mradi mpaka leo umechelewa kwa siku 477. Nikawaambia mbona mtaani mimi nilikuwa sijui Wabunge/wananchi wanajua? Wakasema hatujawaambia kazi yangu ya kwanza ilikuwa kwenda kwenye Kamati na kuwaambia ukweli kwamba kwa mujibu wa wataalam mradi umechelewa na sababu ni hizi. Kwa sababu, huu mradi sio wa kwangu binafsi ni mradi wa nchi na ninapowaeleza Wabunge na Kamati nataka tusaidiane namna ya kutoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo linatupwa kama zigo la Waziri in fact katika hizi changamoto tulizozisema, zimetokana na sisi kubadilisha mfumo wa usimamizi wa mradi ule. Leo hii mkandarasi yule anasimamiwa kwa ukaribu kuliko ambavyo amewahi kusimamiwa siku zote sisi jukumu letu ni kuhakikisha kwamba, mradi huu unakwisha ukiwa salama na ukiwa imara na hicho ndicho tutakachofanya na hicho ndicho tunachoendelea nacho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna mengine ya REA tutaendelea nilivyozungumza naomba kauli yangu niliyoitoa hapo nyuma kwamba tunakwenda kwenye vitongoji. Tumeyapokea maoni ya Wabunge kuhusu hii classification ya miji na vijiji tutakwenda kuifanyia kazi vizuri tuje tutoe tamko sahihi, tutakuja na mpango wa kupeleka umeme kwenye vitongoji. Kuna fedha nyingi tumepata karibu shilingi bilioni 400 ambazo zitatupeleka kilomita mbili mbili sasa, kwa Kijiji kuliko kilomita moja moja kama kwenye REA II round III. La mwisho kabisa… (Makofi)

MWEYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe hoja moja ya mwisho. Hapa ninayo taarifa ya TRA ya mapato ya quarter ya nne ya 2020 na quarter ya nne ya 2021. Ukiangalia mapato ya TRA kwa Novemba 2020/2021 ilikuwa ni shilingi trilioni 1.3, Novemba mwaka huu ni shilingi trilioni 1.7 imeongezeka. Ukiangalia mapato ya mwaka juzi Disemba yalikuwa shilingi trilioni 20.0 mwaka huu ni shilingi trilioni 2.4 sehemu kubwa ya mapato inalipwa na watu wanaozalisha shughuli za viwandani. Ukiangalia growth ya quarter ya mwaka jana ya mwisho na growth ya quarter ya mwaka huu wa mwisho kuna ongezeko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna hii steria kwamba hali imedondoka uchumi umeharibika nenda kwenye takwimu za mapato na hawa ni watu wa viwandani. Sisi tumefanya hivyo kwa sababu tunajua kwamba katika changamoto hii lazima uwapelekee umeme pia watu wa viwandani na watu wa mitaani. Huku pia na wenyewe wapunjike wakati wengine wa mitaani wanapata wa viwandani wanakosa ndivyo inavyokwenda. Tungeweza kabisa kuwaambia watu wenye viwanda vitatu funga viwanda funga mdomo umeme, tupeleke mitaani watu wafurahi lakini haya mapato ya kodi yasingepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeamua kufanya hivyo kwa maslahi ya nchi vile vile lakini tunajua jukumu letu kubwa, ni kuongeza uzalishaji wa umeme kuimarisha miundombinu ya usafirishaji na usambazaji. Kazi hiyo tutaifanya tunaiweza tunayo maarifa tuna-management nzuri ya TANESCO tuna bodi nzuri ya TANESCO; na ninataka nilihakikishie Bunge hili na watanzania kwamba watupe muda watupime kwa matokeo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii ya kuchangia hoja hii na moja kwa moja nianze kusema kwamba naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Kigua. Ni hoja iliyokuja kwa wakati sahihi kwa jambo sahihi na kwa namna sahihi. Pia nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na kutoa maoni katika hoja hii. Maoni, ushauri,
mapendekezo mazuri kabisa, nasi kama Serikali tunayachukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mambo kadhaa katika jambo hili. Ni dhahiri kwamba, wote tunajua bei zimepanda duniani. Nasi kama nchi sio wazalishaji wa mafuta, tunanunua mafuta kutoka nje na sehemu kubwa ya bei ya mafuta inayopangwa hapa Tanzania inatokana na vitu viwili. Kwanza, gharama ya mafuta yenyewe kwenye Soko la Dunia; pili, gharama ya kuyaleta mafuta hapa Tanzania; tatu, kodi na tozo mbalimbali za hapa nchini; na mwisho kabisa, gharama za kufanya biashara yenyewe hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna mambo katika hayo hatuna mkono nayo. La kwanza ni bei ya mafuta duniani; la pili, ni gharama za kuyaleta mafuta duniani na la tatu ni gharama ya ufanyaji wa biashara yenyewe ya mafuta. Sasa tunaweza kusema maana vita ya Ukraine imekuwa ndiyo sababu ya rahisi zaidi. Siku hizi wanasema, mtu hata ukichelewa kurudi nyumbani unasema vita ya Ukraine. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii vita imesababishaje? Kwa sababu ni lazima kulieleza. Ukilieleza hivi juu juu tu, hata wananchi wanasema kila kitu sasa mnasema vita. Asilimia 12 ya mafuta yote duniani yalikuwa yanazalishwa na nchi ya Urusi. Ni nchi ya pili kwa uzalishaji wa mafuta; ya kwanza ni Marekani; ya pili ni Urusi na Saudi Arabia wanakaribiana. Asilimia 12 ya mafuta yaliyokuwa yanazalishwa Urusi yalikuwa yanauzwa pale eneo la Ulaya. Baada ya vita sasa, kwanza uzalishaji ukapungua; pili, mauzo ya mafuta Ulaya na yenyewe yakasimama, kwa sababu zile nchi zilipunguza kununua mafuta na sasa hivi zinataka kugomea kabisa.

Mheshimiwa Spika, mfumo wa usafirishaji wa mafuta yale katika nchi za eneo lile ulikuwa ni karibu. Sasa hivi ambapo yale mafuta yanatafuta soko alternative, mfumo mzima wa usafirishaji wa mafuta duniani maana yake ni kwamba meli hizi zinaenda umbali zaidi, insurance inakuwa kubwa zaidi nagharama inakuwa kubwa zaidi. Kwa hiyo, siyo suala la bei tu, hata suala la usafirishaji wa mafuta limekuwa kubwa sana na ndiyo maana premiums, maana gharama ya kuleta mafuta imepanda sana kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, ukitazama hizi bei za mwezi wa Tano ambazo zimepanda kwa kiasi kikubwa ambazo ndiyo zimesababisha hoja hii, maana yake ni kwamba zimetokana na bei iliyokuwepo ya mafuta duniani miezi miwili iliyopita. Mfumo wetu sisi ni kwamba bei ya mafuta tunayoingiza ambayo yamesafishwa ya kwenye pump hapa nchini, bei zake zinashabihiana na bei za dunia za miezi miwili iliyopita.

Mheshimiwa Spika, mtu akiangalia kwenye internet leo akaona bei zimeshuka, akasema ninyi hamshushi, inakuwa ni makosa, lazima utazame bei za miezi miwili iliyopita ndiyo ujue bei ya pump leo. Ukitazama historia ya bei ya mafuta duniani kwa miaka 15 iliyopita, bei ya juu iliyowahi kufikiwa miaka 14 iliyopita ilikuwa ni Shilingi 137/= kwa pipa. Sasa hivi bei ya mwezi Machi ilikuwa ni kubwa kuliko bei ya miaka 14 iliyopita. Ndiyo maana bei za mwezi wa Tano zimepanda kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuna mengi ya kueleza kuhusu kupanda kwa bei. Sasa nini tunafanya, kwa sababu muda ni mfupi?

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais, alitoa maelekezo na Mheshimiwa Waziri Mkuu jana tumekaa kikao kirefu kutazama hatua za haraka kama ambavyo Wabunge wanataka tufanye, kama ambavyo wanawasilisha sauti za wananchi wanaowawakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hatua ambayo imezungumzwa kwa kirefu nayo ni ya kikodi na tozo. Sasa hizo hatua zinataka mashauriano, zinataka uzingatiaji wa sheria na kanuni zinazoongoza uwekaji na uondoaji wa hizo kodi na tozo. Sasa bahati nzuri mamlaka yapo kwenye Serikali, lakini pia mamlaka yanayohusu masuala ya kifedha pia yapo hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi kama Serikali na kama alivyogusia Mheshimiwa Simbachawene, tunasema kwamba suala hili tumelichukua. Tunafahamu udharura na uharaka wake, na vilevile tunataka uzingatiaji wa sheria, kanuni na taratibu za nchi zinazohusiana na masuala ya kodi. Hivi karibuni tumekubaliana kwamba tutakuja na majawabu kuhusu suala hili, hasa kwenye masuala haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kama alivyozungumza Mheshimiwa Waziri Mkuu jana, suala lingine ni kutafuta namna mbadala ya kupata watu watakaotuletea mafuta kwa bei nafuu. Suala hilo limetokana na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge hapa Bungeni, nasi tukatoa kauli kukaribisha watu. Tumepokea maombi mengi, tumeyachakata na tuna imani kabisa kwamba katika wale ambao watapita vigezo ambavyo vitazingatia kanuni na taratibu na sheria za Serikali, tutaingia nao kwenye mazungumzo kwa namna ya uwazi, ili tuone kama tunaweza kupata nafuu katika uagizaji huo wa mafuta.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema wakati ule, sisi hatung’ang’anii mfumo hata kama hautupi bei nzuri. Kama Serikali tupo tayari kwa njia yoyote kwa namna yoyote kutumia mfumo wowote ambao utatuhakikishia bei nafuu na hilo ndilo ambalo tumelifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na malalamiko kuhusu mfumo uliokuwepo. Malalamiko haya yamekuwepo muda mrefu, lakini pia biashara ya mafuta ni biashara ambayo ina vita ya wenyewe kwa wenyewe. Kuna madaraja matatu; kuna wenye vituo, kuna wa katikati wale MCS na kuna wale suppliers. Huu mfumo umekuwa ni sehemu ya ugomvi; na wakati mwingine udhaifu wa mfumo pamoja na kwamba upo wakati mwingine unakuzwa ili mfumo huu aidha uchanganywe na vitu vingine au uondolewe kabisa ili turudi kule katika mfumo ambao ulikuwa hautuhakikishii supply. Falsafa yetu ni kwamba chochote kinachotuhakikishia bei nafuu kuleta mafuta tutakifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa pamoja na kwamba tunachukua hizi hatua za kikodi haraka zaidi lakini kuna hatua za muda wa kati ambazo pia tumeanza kuzichukua. Mojawapo ni kuanzisha hifadhi ya kimkakati ya Taifa ya mafuta (Strategic Petroleum Reserve). Iliahidiwa muda mrefu na mimi nimeelekeza na ndani ya wiki mbili tutasaini kanuni mpya kwa sababu lazima ianzishwe kwa kanuni inayotokana na Sheria ya Mafuta ya Petrol ndani ya wiki mbili tutaanzisha kanuni mpya za kuanzisha hifadhi ya kimkakati ya mafuta hapa nchini, na tutaelezea kwa kirefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hatua nyingine ni kuanzisha mfuko wa kuhimili bei za mafuta kama alivyozungumza Mheshimiwa Shangazi, inaitwa Fuel Price Stabilization Fund. Wizara ipo katika hatua za mwisho za kuandika andiko la Baraza la Mawaziri na tutapeleka katika kikao kijacho cha Baraza la Mawaziri ili mfuko huo uanze na uweze kutumika katika nyakati kama hizi kwa siku zijazo; na utaratibu wake tutauelezea kwamba mfuko huu unapataje pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nyingine ni ile ndoto yetu ya muda mrefu ya kuanzisha kituo kikubwa cha biashara ya mafuta hapa nchini. Pia tuko katika hatua za mwisho, kwa sababu hii ina ushirikiano na sekta binafsi, wa kuigeuza TIPPER kuipanua, kuikarabati, kui-modernize na kuijengea uwezo wa kuhifadhi mafuta mengi zaidi na ili pale sasa pawe kituo kikubwa cha biashara ya mafuta katika ukanda huu.

Mheshimiwa Spika, ndani ya mwezi huu wa tano kabla haujaisha tutasaini makubaliano na sekta binafsi ya kuanzisha kituo hicho kitakachotuwezesha kuhifadhi mafuta yatakayotosheleza mahitaji ya hapa nchini kwa kipindi kirefu.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kwamba, rasmi kama Waziri mwenye dhamana nimeongea na Mawaziri wenzangu katika ukanda huu wa Afrika Mashariki pamoja pia na nchi za Zambia na Malawi kuomba tuitishe mkutano wa dharura ndani ya mwezi huu wa tano kule Arusha ili kwa pamoja tujadiliane kama tunaweza kuunganisha nguvu na kujenga soko moja la ukanda huu ili tuwe na mkono mkubwa zaidi wa kuweza kuamua namna ambavyo tunaweza tuka-dictate bei vilevile. Tumeshakubaliana kikao hicho kitafanyika Arusha. Bado tunazungumza kuhusu tarehe kwa sababu yapo ya kubadilishana uzoefu.

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile ni ile point aliyoongea Mheshimiwa Manyanya kwamba mafuta hapa duniani yapo ya kutosha chini ya ardhi yanayoweza kutolewa kwa ratiba stahiki na bei ikashuka, lakini kuna mambo ya kijiopolitiki, mambo ya kisiasa duniani ambayo yanasababisha baadhi ya mafuta yawe locked out kwenye soko la dunia. Lakini mkiunganisha nguvu kama nchi kama za kwetu mnaweza mka-lobby na mkafanya jitihada ili mafuta ya namna ile yaingie kwenye soko la dunia na bei iweze kushuka. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya Mheshimiwa Waziri malizia dakika moja.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, la mwisho tumekuwa tunafanya jitihada; nimeongea na Waziri wa Algeria, Waziri wa Nishati wa Zabeijan, Waziri wa Nishati wa Oman kuona kama tunaweza kwa nchi kupata unafuu. Na katika mazungumzo yote jambo moja limekuja kwamba Mheshimiwa Waziri tunaweza tukawapa petrol diesel hatuna. Kwa sababu hapa imezungumziwa habari ya diesel, tofauti ya diesel. ukitazama mwenendo wa bei katika mwaka mzima uliopita landed cost ya mafuta bei iliyofika pale Dar es Salaam, ukiangalia jirani zetu Wakenya mwezi Machi tofauti kati ya gharama za diesel ilipofika Kenya na petrol ilipofika Kenya kuna tofauti ya shilingi karibu 600 kwa Kenya.

Mheshimiwa Spika, hapa kwetu landed cost ya diesel na petrol ilikuwa ni 1,960 kwa petrol, 2,150 kwa diesel. Kwa mara ya kwanza unaona divergence (kupanuka) kwa tofauti kati ya diesel na petrol. Leo hii kituo kikubwa (price point) ya diesel duniani ni Bandari ya New York. Kwa mara ya kwanza diesel iko chini kwa record ya miaka 32 iliyopita na nchi yetu hii siyo mara ya kwanza ambapo diesel iko juu kuliko petrol. Yote inahusiana na mfumo wa usafirishaji wa diesel na petrol na refining capacity na demand ya diesel na petrol.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kusitokee maneno hapa kwamba petrol iko hivi kwa hiyo kuna kitu, hili ni jambo la kawaida katika biashara hiyo. Napenda nihakikishie Bunge lako kwamba Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan inawajali wananchi, inajua kilio chao inaungana na Wabunge katika kuhakikisha kwamba kilio hicho cha kupunguza gharama tunakichukua na tunakifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalize kwa kuunga mkono hoja tena. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, inaelekea Waheshimiwa Wabunge wanataka twende kwenye Kamati ya Matumizi moja kwa moja, lakini kwa kuwa kuna masuala waliuliza na waliyachangia basi kwa heshima na taadhima na kwa kibali chako ningependa kujielekeza kwenye baadhi ya hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nitoe shukrani kubwa sana kwako na shukrani kubwa na nyingi kwa Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii kwa kuzungumza na kwa maandishi. Tumefarijika sana kwa sababu michango ni mizuri sana, michango iliyotupa elimu kubwa, iliyotuhamasisha, iliyotutia moyo, iliyotuelimisha, iliyotufikirisha. Kwa hiyo tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa kweli kwa kuitendea haki hoja yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliochangia ni wengi, wamezidi 70, nadhani ni rekodi katika hoja za hivi karibuni, na hatutaweza katika muda huu tulionao kutoa majibu yote na kwa wote; ila tumefanya jambo kidogo tofauti kwamba mkienda kwenye visimbuzi vyenu tayari hivi ninavyozungumza majibu tumeshayatoa kwa Waheshimiwa Wabunge wote. Nimshukuru pia Naibu Waziri naye kwa kunisaidia na kusaidia kujibu baadhi ya hoja vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nijielekeze kwenye baadhi ya mambo yaliyozungumzwa na Wabunge wengi kwa makundi. Kwanza ni kuhusu suala la LNG. Hili ni jambo kubwa sana, na sisi tumefarijika kwamba Waheshimiwa Wabunge wengi wamelizungumzia. Katika bajeti yetu hii, kutokana na nchi yetu kuingia kwenye mradi huu Bajeti ya Wizara ya Nishati inatazamwa na Dunia ya Nishati. Kwa sababu Mradi wa LNG Tanzania ni mradi wa usalama wa nishati duniani; ni Global Energy Security Project. Kwa sababu hii gesi inapelekwa kwenye masoko ya nchi kubwa zenye viwanda zilizoendelea zenye njaa ya nishati, kwa hiyo uhakika wa upatikanaji wa gesi hii ni suala linalotazamwa na wengi. Kwa hiyo wenzetu dunia nzima walikuwa wanatazama Tanzania tunasemaje kuhusu huu mradi?

Mheshimiwa Spika, lakini siyo bajeti yetu tu, hata michango ya Wabunge ilikuwa na yenyewe inatazamwa. Je, hao wawakilishi wa wananchi na wenyewe wanasemaje? Huu mradi wanauchukuliaje? Naomba niwape mrejesho kwamba wenzetu wamefarijika sana kwamba kuna hamasa kubwa, kuna uelewa mkubwa na kuna hamu kubwa miongoni mwa viongozi wa nchi yetu, kwa sababu ninyi ndio viongozi, kuhusu mradi huu. Kwa hiyo tumefarijika sana kwa mchango wenu na umetupa nguvu sisi tunaosimamia mradi huu kwamba si mnaona? Mradi huu una support ya wananchi kupitia wawakilishi wao. Kwa hiyo tunapenda niwashukuru sana kwa hilo na tutapenda pia kuwaomba katika hatua zinazokuja ikiwemo sheria mahususi ya mradi huu; kwa sababu kama nilivyoeleza kwenye hotuba yetu tutatengeneza project law ya LNG tutaleta Bungeni hapa sheria mahususi ya mradi ili muone vitu gani vitasaidia kuendesha mradi huu ili uwe na tija na manufaa na maslahi kwa nchi. Kwa hiyo Bunge litakuwa na nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba pia tutakapokuja wakati huo pia moyo mliouonyesha katika hatua hii pia muendelee kwa sababu wataendelea kutazama. Kwa hiyo nawashukuru sana sisi tumeyapokea ushauri mlioutoa kwamba tuharakishe utekelezaji, na tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni suala la kukatika katika kwa umeme. Hili Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza, na labda niseme tu kwamba suala hili ni changamoto ya muda mrefu. Kwenye bajeti yetu lilizungumzwa pia na siku za nyuma pia limezungumzwa. Tunafarijika kwamba sasa hivi ni kwa maeneo mahususi. Kwenye bajeti ya mwaka jana ni Wabunge wengi zaidi lilikuwa linawagusa katika maeneo yao, lakini kadiri muda unavyoenda maeneo yanapungua, hatusemi tumemaliza lakini maeneo yanapungua.

Mheshimiwa Spika, hili suala ni la kihistoria, labda nichukue muda kulieleza kidogo. Utakumbuka kwenye miaka ya 1990 nchi yetu iliingia kwenye hamu ya ubinafsishaji wa mashirika ya umma. Na ikawa ikiamuliwa kwamba shirika libinafsishwe linawekwa kwenye kundi la makampuni yanaitwa specified na linakuwa gazetted kabisa. Na ikishaamuliwa hivyo, Serikali inasimamisha uwekezaji katika shirika hilo na inasimamisha hata ajira. Kwa hiyo moja ya shirika mwaka nadhani 1993/1994 lililowekwa kwenye kundi la ubinafsishaji ilikuwa ni TANESCO miaka hiyo. Baada ya uamuzi ule kufanyika ajira zilisimama, uzalishaji wa umeme ulisimama, ujenzi wa miundombinu ulisimama, ukarabati wa miundombinu ulisimama kwa sababu tulikuwa tunasema tutalibinafsisha.

Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya uamuzi wa kulibinafsisha ukachukua muda mrefu, takribani miaka 10 haukufanyika. Baadaye uamuzi ulipofanyika ulikuwa hatubinafsishi tena, libaki shirika la umma. Lakini katika kipindi ambacho uamuzi huo ulikuwa unatafakariwa, ni kipindi ambapo uchumi ulikuwa una kua kwa kasi sana, idadi ya watu inaongezeka, tumefungua uchumi wetu kwenye dunia na wawekezaji wanakuja. Kwa hiyo katika kipindi ambacho uzalishaji wa umeme umesimama, ujenzi wa miundombinu umesimama ndipo ambapo nchi ilikuwa inaenda mbele kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ile historia ya miaka 10 ya kutokuwa na ukarabati, uwekezaji wala uzalishaji malipo yake ndiyo tunayalipa sasa. Ndiyo, kwa hiyo lazima historia tuwe nayo sahihi. Sasa kwenye umeme, kama nilivyosema, kuna uzalishaji wa umeme, kuna usafirishaji kwenye yale mawaya makubwa na kuna usambazaji. Hivi vitu vyote lazima viwe sawa ili uweze kupata umeme wa uhakika. Tukiwa wakweli wa nafsi zetu, na kwa sababu sisi ni viongozi tuna wajibu wa kusema ukweli, hatukuwa na umeme wa kutosha. Nchi yetu yenye watu milioni 60, sisi tunao safiri duniani ukiwa Waziri wa Nishati swali la kwanza vipi mna megawati ngapi na kule wanatumia gigawatt, 1,800 wanasema 1.8 gigawatt.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nchi yetu tunasema tuna umeme 1.8 gigawatt. Mimi huwa nawaambia watu wangu tusitumie neno gigawatt, tutumie neno megawatt angalau zionekane nyingi, 1,800. Kwa sababu kwenye nchi nyingine umeme wa nchi yetu 1.8 gigawatt au megawatt 1,800 ni umeme wa sehemu kama Kisesa, mtaa sio umeme wa nchi. Sasa kwenye nchi ambayo ina malengo makubwa ya maendeleo kama yetu, watu wanaongezeka kwa kiasi kikubwa, shughuli zinapanuka, lazima tuondoke katika hali hii. Na katika uamuzi wa kijasiri uliowahi kufanyika katika nchi hii ni uamuzi uliofanywa na Rais wa Awamu ya Tano ya kujenga Bwawa la Julius Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ule utatupunguzia aibu ya kusema 1.8 gigawatt. Na ilani yetu imetuelekeza kwamba ifikapo 2025 walau tuwe tumefika 5,000; 5.0 gigawatt. Bado, bado. Na sisi sasa hivi tunadhani tuna umeme wa kutosha, lakini ni kwa sababu; ninaenda kwenye jambo la pili la usafirishaji na usambazaji; umeme huu tunaona unatosha kwa sababu haujawafikia wote wanaouhitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo tunaingia jambo la pili, la miundombinu. Leo hii tukiweza kutimiza mahitaji ya Mheshimiwa Dotto Biteko na wamezungumza Wabunge wa Geita, Wabunge wa Kahama rafiki zangu Kassim na Cherehani na Dada Rose pale. Tukiweza kuipa migodi yote inayotumia diesel leo umeme ni megawatt 1,200 kwa mpigo. Naomba nirudie. Tukiweza kuipa migodi yote nchini sasa hivi inayotumia diesel tukiweza kuipa umeme itatumia umeme sawa na umeme wote tulionao siku ya leo, mwaka huu katika kipindi hiki. Maana yake ni kwamba bado hatujawafikia Watanzania wengi wanaohitaji umeme, acha kwenye nyumba hata kwenye maeneo ya kilimo, uzalishaji na migodi.

Mheshimiwa Spika, usambazaji; umeme unaenda kwenye mitaa yetu na kwenye wilaya zetu. Na kitaalamu umeme wa usafirishaji una nyaya zake, umeme wa usamabzaji una nyaya zake. Nyaya za umeme wa usambazaji ni za bei nafuu, za usafirishaji ni za bei ghali. Sasa ili huko nyuma tuweze kupeleka umeme kila mahali, tukawa tunasafirisha umeme kwa njia za usambazaji. Matokeo yake Mheshimiwa Simbachawene pale, line inayotoka hapa Zuzu inaenda Mpwapwa, inaenda Kongwa, inatokea Gairo inaenda Kiteto ni line hiyo hiyo moja kilometa zaidi ya 1,000 wakati ilipaswa kwenda kilometa 100 tu.

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kwamba nguzo ikianguka hapo Mvumi huko kwenda umeme unakatika mpaka Kiteto. Sasa ndiyo changamoto tuliyonayo na ndio ukweli wenyewe na ni maeneo mengi. Tabora pale mji mzima wa Tabora una waya mmoja tu mrefu, mpaka Urambo, ulikuwa ni waya huo huo mmoja kilometa 1,200. Sasa Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita alivyoingia madarakani akatupa hii kazi umeme ukawa unakatika tukaanza kunyoshewa vidole, ni yule Bwana Kipara pale ndiye anakata umeme. Ni Bwana Maharage pale ndiyo anakata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tulichofanya tukakaa tukajifungia na wataalamu wale mnaowaona tukawaambia hebu tuambieni ukweli. Maana kulikuwa na dhana kwamba ni hujuma. Mimi siamini kabisa mtu ameajiriwa TANESCO ahujumu kukata umeme kuzima umeme kwa sababu ndiyo maisha yake. Ndipo wakasema wakuu, unajua Serikali tunaitana wakuu. Wakasema mkuu, nikwaambia hebu acheni mambo ya mkuu, hebu semeni tu kinachoendelea. Ndipo tukapewa uchambuzi wa hali ilivyo, na sisi tukapendekeza mpango mahususi mkubwa, unaitwa Grid Imara, wa gharama kubwa sana wa kubadilisha nyaya za zamani kuweka nyaya nene zaidi. Pia kuvalisha nguo zile nyaya, kubadilisha transformer, kujenga na line nyingine mpya. Tukauita Mradi wa Grid Imara wa trilioni 4.4 tukaenda kwa kiongozi wetu Mheshimiwa Rais tukamuwasilishia ule mpango akasema sawa nitawaanzia na shilingi bilioni 500, tukaja Bungeni mkatuidhinishia. Tukaenda tukaanza awamu ya kwanza tukatafuta wakandarasi 26 sasa hivi miradi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,Hii ni safari. Sitaki kuwadanganya kwamba umeme utaacha kukatika mwakani au mwaka unaofuatia. Ambacho nawaahidi tumeweka jitihada kila mwaka tutakuwa tunapunguza changamoto hii. Mpaka mpango huu ukamilike. Hakuna watu wanaoumia kunapokuwa na changamoto ya kukatika kwa umeme kama sisi tunaosimamia sekta kama wataalamu kule TANESCO. Kwa hiyo tunafahamu madhara kwa uchumi, kwa vifaa vyetu kutokana na kukatika kwa umeme ila naomba muiamini Serikali. Na mimi ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais, mara moja alielewa, mara moja aliridhia, mara moja aliidhinisha na Bunge hili tunalishukuru kwamba mara moja na nyie mlielewa na mara moja mliridhia na mkaidhisha ule mpango.

Mheshimiwa Spika, tunaomba sasa, mwaka huu tumeomba zaidi shilingi bilioni 400 zaidi kwa kuendelea na ule mpango. Kwa hiyo sasa sisi hapa nchini ili umeme uwe imara walau kila wilaya iwe na kituo cha kupozea umeme (substation). Ninyi mnatoka huko wilayani, nchi nzima kuna vituo 46 tu, wilaya 46 tu ndizo zina vituo katika wilaya zetu zote. Tumekuja na mpango mwingine wa kujenga substation kwenye kila wilaya.

Mheshimiwa Spika, safari ya kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme itakuwa ni safari siyo tukio, ni safari. Tunachoomba ni subira na uvumilivu; na wakati mwingine tupeane nafasi.

Mheshimiwa Spika, siku moja hapa umeme umekatika Bungeni kulitokea hitilafu, ghafla bana fukuza Waziri, fukuza TANESCO. Kumbe kuja kuchunguza wala; umeme umekatika kwenye uwanja wa mpira, fukuza Waziri, fukuza TANESCO, kumbe ni mambo mengine. Kukiwa na mkutano watu wakichezea chezea huko umeme ukikatika fukuza. Jamani si wakati wote ni TANESCO na si wakati wote ni Wizara. Sisi tutachukua wajibu wetu pale linapotokea na moja ya hatua ni kuimarisha shirika lenyewe linalofanya kazi hii ili liwe na weledi. Na mmeona mliotembelea pale mabadiliko makubwa yanayoendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwenye hili la kukatika kwa umeme tutapunguza, lakini sitaki kuwaambia kwamba kesho itaisha. Wote tutawapa na tutaweka dash board muingie muone maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa Grid Imara. Tutawapa link muone wapi tumebadilisha, wapi hali imebadilika, wapi tatizo lipo ili muweze na ninyi kufuatilia, ili na nyie mtusaidie kusema kwa wananchi. Hilo tutalifanya katika kipindi cha miezi miwili ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mradi wa Julius Nyerere ni mradi wa kihistoria kama nilivyoeleza na umezungumzwa sana hapa na tunawashukuru sana kwa kuunga mkono. Tulileta ile teknolojia ili muone maendeleo kwa sababu walau inaitwa virtual reality yaani unakaribiana na ukweli wenyewe. Naomba nitoe tangazo hapa kwenye Bunge kwa ridhaa yako, sisi tuko tayari, si tu kusafiri kutokea hapa Bungeni kwa kuvaa miwani, kwa ratiba Mheshimiwa Spika atakayoweka, kwa logistics zitakavyokuwa tuko tayari kuwasafirisha Waheshimiwa Wabunge wote kwenda kwenye mradi mkauone wenyewe wakati wowote ili tusiishie hapa; na hilo tutaongea na Ofisi ya Mheshimiwa Spika ili tuweze kuliweka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kuna suala la mradi umechelewa, mradi umechelewa, mradi umechelewa, kwa nini hatujamkata mkandarasi limezungumzwa. Miradi hii ya kuzalisha umeme kwa kutumia maji ina ukubwa tofauti. Huu ni mradi mkubwa katika ukanda huu. Mkataba wa kwanza ulikuwa miaka mitatu ya ujenzi lakini ukiangalia miradi mingine, ukienda Kihansi, Mtera, Hale, Pangani Falls hamna mradi kati ya hiyo na ni midogo megawati 80, megawati 200, 180 hakuna uliojengwa chini ya miaka mitano. Naomba nirudie, mradi wa megawati 80 hapa Mtera umejengwa miaka sita.

Mheshimiwa Spika, mradi wa Julius Nyerere sisi tulipanga kuujenga; fikiria ni megawati 2,000; tulipanga kuujenga kwa miaka mitatu. Sasa CAG alitusema kwamba hakukuwa na ukadiriaji sahihi wa muda wa ujenzi wa mradi, na alikuwa sahihi kabisa. Hakuna mahali popote unaweza kujenga megawati 2,115 kwa miaka mtatu, hakuna. Kwa hiyo ndio ukweli. Mchungu lakini ndiyo ukweli. Sasa muda umeongezeka, muda ukiongezeka mkataba uliowekwa una namna za kushughulikia mambo hayo ndani ya mkataba. Hadi leo hatujavunja mkataba kwa sababu hata hiyo nyongeza imeelezewa ndani ya mkataba itafanyikaje.

Mheshimiwa Spika, kuna habari kwamba watu wanakwenda mahakamani si kweli. Na kuhusu malipo kwa hiyo nyongeza. Kuna hoja hapa kwa nini hamumkati mkandarasi kwa kupitisha muda. Hiyo dhana ya kumkata siyo sahihi kwa sababu fedha tunazo sisi si kwamba anazo yeye, tunazo sisi. Sasa haki ya kubaki nazo hatujaipoteza. Naomba nirudie, haki ya kubaki nazo hatujaipoteza. Ilikuwa ni suala la busara, tu kwamba je, ile Juni mwaka jana mradi ukiwa asilimia 60 ndipo ufanye fujo wakati ule? Au utumie busara usiipoteze haki yako mradi usonge mbele hadi huko mbele? Kwa sababu hupotezi ile haki mpaka siku ya mwisho.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna baadhi ya watu hapa wanasema hakuna kamata hao, zuia, zima, ondoa, leta mwingine. Mnajua mobilization ya mkandarasi mpya pale inavyokuwa?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo wakati mwingine maarifa, weledi, mkakati unahitajika kusimamia hii miradi mikubwa. Mradi leo uko asilimia 87 haikutokea kwa ajali imetokea kwa maarifa, kwa weredi na kwa mkakati, hakuna hata siku moja kazi imesimama pale na mambo yanaendelea. Kwa sababu tumeamua kutofautisha, kushughulikia mikataba na kusimamia mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu pia ulianza pia kama sehemu ya mahusiano kati ya nchi na nchi, marais wawili walizungumza, kwa sababu ni mradi mkubwa. Mkandarasi kutoka Misri, haiwezekani mkandarasi kutoka Misri wa mradi mkubwa kama kuu viongozi wasiwe na mahusiano katika kuuzungumzia. Kwa hiyo pia mradi huu unalelewa na mahusiano mazuri yaliyopo kati ya nchi zetu mbili Misri na Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tangu mimi nimeingia katika nafasi hii Mheshimiwa Rais wetu amekutana na Rais wa Misri mara tatu na mimi nikiwepo. Mheshimiwa Rais wetu ametuma Mjumbe maalum Misri kwa barua maalum kuhusu mradi na Rais wa Misri ametuma Mjumbe maalum hapa kuhusu mradi huu. Kwa hiyo mradi huu pia unalelewa na mahusiano kati ya nchi zetu mbili, hauwezi kufeli. Na katika kushughulikia mradi huu lazima tulizingatie na hilo, hatuwezi kuliacha; ndiyo maana hamna mambo ya Mahakamani haitotokea. Juzi tu tumepokea mjumbe maalum pia mwingine wa Rais wa Misri kuhusu mradi huu. Kwa hiyo naomba mtuamini, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeweka sayansi ya usimamizi wa miradi, tunaizingatia, tumefika pazuri sana, mradi huu utakwisha salama kwa kibali cha Mwenyezi Mungu na tutawapeleka mkaone, mtafurahi na mtapata fahari ya uwezo wa Watanzania wenzenu kufanya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mambo ambayo yanapaswa kutuunganisha Watanzania ni huu mradi. Hii dhana kwamba kuna watu wanataka kuhujumu, kuna watu hawautaki, kuna watu wamefanya kosa hapa, kuna watu nini na nini; mimi naomba huu mradi tusiutumie kupata sifa ya siasa kabisa. Kwamba mimi ndiyo mbabe zaidi, ndiyo naweza kuusimamia kuliko watu wote waliyopewa dhamana ya kusimamia mradi huu. Naomba siasa iwekwe pembeni na mradi huu kabisa, mradi huu ni mkubwa wa heshima na wa bei kubwa sana kwa fahari ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu CSR imezungumzwa hapa ni sehemu ya makubaliano ya mradi huu. Tulikubaliana wakati tunausaini kwamba asilimia 3 itatumika kwa miradi ya kijamii, lakini tukimlipa kwa wakati kwa miaka miwili tutapata asilimia moja ya ziadi, kwa hiyo imekuwa asilimia 4 ambayo ni sawa na shilingi bilioni 262. Sasa zile fedha kwenye yale makubaliano kulikuwa na makubaliano zitumike wapi? elimu na afya lakini baadaye ukafanyika uamuzi kwamba hapana tujenge uwanja wa mpira na barabara.

Mheshimiwa Spika, sasa tukakorofishana na mkandarasi kwa sababu yeye alisema siyo mkataba. Kwa hiyo kile kipindi cha mabishano kilikuwa kirefu mno na hatukufikia mwisho ndiyo maana miradi hii imechelewa kwa sababu kuna sababu mbona hamjafanya? mbona mmechelewa? kwa sababu sisi wenyewe tuliamua kuamua tofauti. Kwa hiyo tukabishana tukaenda mbele, nyuma baadaye busara ikatamalaki kwamba jamani ee pia afya na elimu ni muhimu. Kwa hiyo turudi kwenye makubaliano ya awali, hapo muda ulikuwa umeisha kwenda pia vilevile.

Mheshimiwa Spika, baada ya pale sasa vikaanza vikao, na kwa sababu ni elimu na afya sisi tukatafuta vikao na wenzetu, kwamba jamani nyie sekta ya elimu, sekta ya afya vitu gani muhimu kwenu ili tuweze ku-finance huu mradi? Tukaletewa vyuo vya juu vya ufundi na maeneo tukaletewa na kwa sababu yalikidhi haja na kwa sababu katika vyuo hivi watasoma vijana wote wa Kitanzania kutoka kila kona ya Tanzania. Sisi suala la pahala hatukuliona ni suala kubwa, kiwe Rufiji, kiwe Dar es salaam, kiwe Morogoro kama chuo cha UDOM hapa kipo Dodoma lakini asilimia ngapi ya watu wa Dodoma wanasoma hapa? Watanzania wote wanasoma pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tukaona kwamba tusiingie kwenye changu, changu, leta kwangu na nini? ila kitu ambacho tunakili ni kwamba wenzetu ambao mikoa yao, wilaya zao, maeneo yao yapo kwenye mradi wanao wajibu mahususi, wanayo majukumu mahususi. Kwa hiyo pia tutazingatia hilo vilevile. Pamoja na kwamba imeamuliwa kwamba tujenge hivi vyuo vikuu vitatu vya juu vya ufundi siyo VETA juu ya VETA very technical lakini tutafanya Morogoro, Pwani na kwingineko tutafanya vitu kwenye afya na kwenye elimu kwa sababu hatuwezi kutoka hapo. Kwa hiyo katika fedha upya tumewasikia Mheshimiwa Kalogeris tuandikieni, Waheshimiwa Pwani vilevile nimemuona Kuchauka naye anasema Liwale pia ni Rufiji sawa na yeye tumepokea, tumepokea kuhusu miradi mingine ya elimu na afya katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja kwamba hii fedha ya CSR imeliwa, imeibiwa si kweli, fedha ipo kwenye mkataba na ipo na tayari chuo cha kwanza Lindi tumeishaona mahala, watu wameishakwenda, watu wameishapima, michoro imeishafanywa na Mungu akijalia mwezi wa saba tutaweka jiwe la msingi pale na kazi itaanza kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi kama nilivyosema Mheshimiwa Rais alipokea Mjumbe maalum wa Rais wa Misri akiwa na barua maalum kutoka kwa Rais wa Misri na moja na ya mambo tuliyozungumza ni utekelezaji wa Miradi ya CSR. Kwa hiyo liko hata kwenye ngazi ya juu litafanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la nishati ya kupikia sisi tunafarijika sana kwamba tumefanikiwa. Kama Bunge kama Serikali kupika na namna ya kupika inachukua takribani asilimia 30 ya mazungumzo ya Bajeti ya Nishati. Hiyo haijapata kutokea. Kwa sababu siku zote tukizungumza nishati, tunazungumza mafuta, umeme, gesi. Sasa ukiweza kuingiza ajenda mpya inayowagusa watanzania kwenye masuala ya Serikali umefanikiwa jambo kubwa. Wakati tunaanza sisi ilikuwa ni mashambulizi jambo gani hili na nini? lakini tume – force mpaka nishati ya kupikia ni mjadala sasa hivi. Kwa hiyo tumeanza mjadala, tumekuja tafakuri sasa tunaenda kwenye hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi tumefurahi sana kwamba Waheshimiwa Wabunge wamehamasika, wameelewa, wameibeba ajenda hii kwa sababu inagusa watu wao. Na pia tumepanua wigo wa masuala sisi wanasiasa ya kuzungumzia kuhusu wanawake, kwa sababu nyuma ilikuwa ni unyanyasaji wa kijinsia, uwezeshaji wa kiuchumi, maji. Kwa hiyo masuala ya wanawake tulikuwa tunazungmza siasa na kwenye majukwaa ilikuwa ni narrow, sasa tumeongeza jambo jipya juu ya nishati ya kupikia ambalo tukilifanya vizuri wote tunapata manufaa ya kisiasa, kijamii na kiuchumi. Lakini pia tunamwezesha mtoto wa kike na yeye kufikia pale anapostaili kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili jambo ni gumu, si jepesi ni gumu. Substation tutajenga, umeme tutaweka mkandarasi atapeleka vijijini sijui bwawa litajengwa ni mambo ya kiufundi ukiwa na hela, ukiwa na mkandarasi linaenda. Suala linalohusu tabia, linahusu mazoea, linalogusa kila nyanja siyo jepesi kwa sababu linahitaji elimu sana, uwekezaji mkubwa, mabadiliko ya sera, mtazamo na kadhalika. Kwa hiyo siyo jepesi, linahitaji sisi sote tuunganishe nguvu. Ndiyo maana Mheshimiwa Rais alivyoamua kuongoza jambo hili sisi tumepata Faraja, na ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge na nyie mlipo libeba tumepata faraja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa tumeamua kufanya jambo hili kwa sababu hiyo hiyo, kwamba ni gumu. Wakati mwingine unaamua majambo siyo kwa sababu ni mepesi bali kwa sababu ni magumu ili kupima kiwango na nguvu yenu kama Chama kama Serikali ya kuleta mabadiliko chanya kwenye jamii. Kwa hiyo hili ni kipimo chetu kuchukua jambo ambalo ni it intellectually challenging ni challenging kisera, kiutamaduni lakini linaleta ustawi wa watu. Kwa hiyo ningependa Waheshimiwa Wabunge tulibebe wote ili tuweze kuwasaidia akina mama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na kumpongeza kwa sababu yeye ndiye Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Kitaifa ya kufanya jambo hili. Ametuongoza, tumekaa vikao vinne. Sasa hivi tunayo rasimu ya mwisho ya dira, tunayo rasimu ya mwisho ya mpango mkakati unao elezea hatua kwa hatua nani afanye nini na kwa wakati gani ili tufike kwenye yale maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya asilimia 80 ya Watanzania watumie nishati safi ndani ya miaka 10. Sasa moja ya mathalani tuliyofanya tunataka, tutagawa nishati hii mitungi, tutafunga mifumo ya kupikia kwenye Taasisi zetu mbalimbali hatuoni aibu, hatuogopi kuwapa Waheshimiwa Wabunge nyenzo ya kuhamasisha. Kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wana ushawishi. Ukitaka jambo lako lifike nchi nzima kwa wakati mmoja wape Wabunge kwa sababu wanafanya mikutano na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulisema hata kwenye bajeti mwaka jana, tulitenga na fedha hapa hapa mkapitisha ya mitungi laki moja. Hii tuliyowapa ni sehemu ya mitungi laki moja tuliyoipangia kwenye bajeti. Na utaratibu wa manunuzi umefanyika watu wameshindanishwa. Mtapata mitungi, kama msambazaji wa Kanda ya Ziwa ni fulani na anauwezo na kanda ile tutafanya, kwa wengine watagawiwa na mtu nyanda za kusini kama kampuni fulani ni u-strong upo. Kwa hiyo wale waliyokuwa wanasema hakuna maeneo ya ujazaji yapo kwa sababu waliyoshinda katika maeneo yenu ni wale wenye mtandao wa usambazaji katika maeneo yenu; kwa hiyo limefanyika, kwa hiyo tutaendelea leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la wafanyakazi wa TANESCO limezungumzwa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa. Naomba niseme tu kwamba Shirika linapitia katika mabadiliko. Kuna masuala ambayo TANESCO tunaka ifanye, kuna matarajio tuliyonayo juu ya TANESCO, lakini vilevile kuna mahitaji ya uchumi mpya ya teknolojia mpya. Sasa, haya mabadiliko niseme wazi hapa hayana nia ya kupunguza mtu, hatutapunguza mtu, hatutapunguza mtu kazi TANESCO. Ila tutawahitaji wawe tayari kupokea ujuzi mpya na majukumu mapya yanayoendana na mahitaji ya dunia mpya vilevile, waondoke katika comfort zone kwasababu dunia ya huduma inabadilika, umeme ni huduma. Kwa hiyo tutawa-retrain, tutawawezesha lakini tutakuwa nao. Mtu ataacha kazi kwa kutaka yeye mwenyewe, hatoondelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na wao wanajua wafanyakazi wa TANESCO, kwa mara ya kwanza katika miaka 17 tumewapandishia mshahara juzi. Miaka 17 hatukupandisha mshahara, sasa hivi tunapimana kwa matokeo, na jam ndiyo dunia ya kisasa, tunapimana kwa matokeo. Kwa hiyo naomba msiwe na wasi wasi mambo yatakuwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu vinasaba tumelisikia lipo Serikalini linashughulikiwa, tutahakikisha kwamba suala hili linakaa mahala ambapo litakuwa na tija na ufanisi.

Mheshimiwa Spika, umeme vitongojini. Waheshimiwa Wabunge hili ni jambo kubwa vilevile, ndoto yetu sisi ni kupeleka umeme kwenye kila kona ya nchi yetu. Mnafahamu vijiji vyote tutamaliza, vimebaki vijiji 2,000. Kila kijiji kina mkandarasi na kazi inaendelea. Lakini kama mnavyofahamu kila kijiji kina wastani wa vitongoji vitano. Kwa hiyo tunaposema tumepeleka vijiji vyote ni maana katika kitongoji kimoja katika vitongoji vitano kwenye kila kijiji. Sasa mtu atakupa kura kwa kumletea umeme karibu na alipo. Kura ukimwambia bana ule palee you know usiwe na wasi wasi umeuona ule tumefanya kazi nzuri; Hapana, lazima uwe pale, na huo ndiyo mwelekeo. Uwekezaji wa kuusogeza ili tuupeleke kwenye vitongoji kwa sababu lazima utue kijijini ili usambae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa sana imefanyika chini ya Serikali ya Awamu ya Nne ya Tano na ya Sita, kazi kubwa sana imefanyika lazima tujisikie fahari kwamba tumemaliza vijiji lakini kazi kubwa ipo mbele yetu. Sasa sisi tulifanya utafiti tulipoingia tu kwenye nafasi hii, ni nini kinahitajika kupeleka umeme vitongoji vyote? fedha, vifaa, muda, rasilimali watu; tukapata huo uchambuzi tukatengeneza mpango lakini kwa kujua kwamba hatuwezi kwenda Hazina kusema haya hiyo tupeni fedha, tukaja pia na maarifa ya chanzo cha kugharamia pia huo mradi. Tukajadiliana ndani ya Serikali na kuchakata na kuangalia mahitaji mbalimbali. Tulikuwa tuanze mwaka huu wa fedha unaokuja lakini busara ikatamalaki kwamba chanzo kile kitumike jambo jingine, mambo mengine muhimu zaidi na sisi tuanze program yetu mwaka kesho kutwa unaofuatia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninapenda niwape Waheshimiwa Wabunge faraja kwamba mpango wa kupeleka umeme vitongoji vyote haujafa tumeuharisha kwa mwaka wa fedha unaokuja tutaenda kwenye mwaka unaofuatia. Ila sasa tumeona basi walau tuwape starter (appetizer) ndiyo maana ya vitongoji vipo kumi na tano. Tunajua havitoshi, lakini sisi vitatusaidia kuangalia utaratibu na namna bora zaidi tutakapofanya ule mradi mkubwa ya kufika. Imani yetu ni kwamba katika vitongoji 15 tutachagua maeneo yenye mahitaji zaidi, maeneo ya huduma, maeneo ya uzalishaji mali, maeneo ya uchumi kwenye minara ya simu na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hii ya vitongoji 3,000 kwa ujumla ukipiga si vidogo kwa sababu mahitaji ni sawa na yale yale ya nyuma ya kupeleka umeme katika vijiji. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge naomba tukubali kwamba tutaendelea na utaratibu wa kujiandaa kwa mwaka unaofuatia. Bahati nzuri sisi tuko tumeishaweka mipango yote ikiwemo namna ambavyo vifaa vitapatikana, namna ambavyo vitasambazwa, utaratibu mpya wa manunuzi tutakapokuja kwenye huo mradi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni masuala mbalimbali ambayo ni mahusisi yaliyozungumzwa. Watu wa Mtwara tumewasikia Msimbati, Madimba kwa kweli tutaleta maendeleo pale kwa sababu hakubaliki kwamba panatoa gesi halafu pako vilevile. Ule mtambo tuliyoahidi kwenda Mtwara umeishafunguliwa mafundi wako Mtwara kazi inaendelea. Wahadzabe Mheshimiwa Flattey nimeona umesema weka historia wapelekee Wahadzabe umeme. Niseme tu kwamba kabla ya Desemba tutawapelekea umeme wa solar uko waliko. Tutaanza na solar kwanza tuone, kwa hiyo tutawapelekea solar. Mheshimiwa Cherehani timu nzima na Mheshimiwa Iddi Kassim timu nzima ya TANESCO na management itakuja Kahama na kukaa na Uongozi wa Mkoa na Wilaya kuangalia mahitaji mahususi ya pale. Cable Zanzibar tutaweka cable mpya Zanzibar ya kutoa umeme Bara na kupeleka Zanzibar. Tunafanya upembuzi yakinifu ili kuongeza uwezo wa umeme kutoka Zanzibar. Naomba nirudie; tutaweka cable mpya ya kupeleka umeme Zanzibar chini ya Bahari. Mheshimiwa Bidyanguze tumepokea, tumesikia waambie watu wako wasiwe na wasi wasi greed Katavi inakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho tu niseme kwamba Waheshimiwa niongee na Wananchi wa Tanzania moja kwa moja kupitia Mheshimiwa Spika kwamba mmewasikia Wabunge wenu na kwa bahati mbaya hapa sikuweza kuwajibu wote ila naomba niwahakikishie kwamba tumewajibu Waheshimiwa Wabunge wenu kwa majibu yanayotatua changamoto walizozisema kwetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kama Waheshimiwa mnatusikiliza, mmemsikia Mheshimiwa Mbunda pale amezungumza umeme, Kapinga kule Mbinga kwa sababu sijamtaja lakini nimemjibu na nimemueleza lini umeme utafika. Kwa hiyo majibu hayo tumeshawafikishia, kwa hiyo msiwahukumu Waheshimiwa Wabungwe wenu kwamba mbona Waziri kasimama hajakutaja. Muda hautoshi ila tumewajibu Wahehsimiwa Wabunge wote.

Mheshimiwa Spika, mwisho kulikuwa na maneno mengi ya faraja kwetu katika mjadala huu; yametutia moyo, tumeyapokea, tumefurahi. Hatukutegemea kwamba Bajeti yetu ingekuwa na hamasa na shamra shamra na pongezi kiasi hiki, tumefurahi. Tumesikia maneno Mheshimiwa Mzee wangu Mzee Deo Sanga, mdogo wangu Mheshimiwa Tauhida kwamba hayo maneno yanayosemwa msiyasikilize kabisa.

Mheshimiwa Spika, sisi tunayasikiliza. Naomba nitofautiane nao, tunayasikiliza kwa sababu yanatusaidia. Tunayasikiliza, hayatutoi relini ila tunayasikiliza. Tunayasikiliza kwa sababu kwanza yanatuongezea umakini. Unajua mtu akiwa anakusema kwa maneno ya uongo, anakusingizia mambo, mnakaa na wenzako jamani mnaona haya. Hebu tusije tukafanya mambo ya hovyo halafu ikaja ikaonekana ni kweli. Kwa hiyo tunashikana, na inatusaidia kuwa makini. Unajua ukiwa unamulikwa unakuwa makini. Kwa hiyo haya maneno yanatufanya saa zote tuwe macho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili haya maneno yanatuongezea hamu na hamasa ya kupata matokeo. Sisi hamasa yetu ni imani ya Mheshimiwa Rais kwetu, hamasa yetu ni matokeo ya kazi yetu kwa uhai wa chama chetu, hamasa nyingine ni kuwasaidia Watanzania kwa majukumu tuliyopewa. Lakini hamasa ya mwisho ni maneno haya, kwa sababu si unataka upate matokeo? Mtu akikusema wewe hufai, maana yake unajitahidi ili uonekane unafaa. Kwa hiyo haya maneno yanatusaidia ndio maana tunayasikiliza. Lakini pia haya maneno yanatusaidia kwa sababu yanawaamsha wanaotupenda na wanaotutakia kheri ili watuombee dua na sala. Kwa sababu ukisemwa sana, rafiki zako, ndugu, jamaa watasema Mungu msaidie, msaidie, wanaamka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hii pia inatusaidia sala na dua zinaongezeka. Kwa hiyo tunayapenda. Lakini mwisho yanatusaidia kwa sababu yanatufundisha kuwa na subira, yanatufundisha kuwa na ukomavu, yanatufundisha kuwa na uvumilivu ili tuwe viongozi bora zaidi. Maneno haya yanatusaidia kwa sababu yanatufundisha ukomavu, yanatufundisha kuwa na subira, yanatufundisha kuwa na uvumilivu na yanatujenga kuwa viongozi bora zaidi. Kwa hiyo sisi tunasema waendelee kwa sababu yanatusaidia.

Mheshimiwa Spika, sisi kisasi chetu ni matokeo, ndio mwisho. Naomba nirudie, hatutabishana, hatutatupa maneno, hatutajitetea, tutalipa kisasi kwa matokeo. Na tunaomba Mwenyezi Mungu atupe afya na uhai tuendelee kuruzukiwa na imani ya Mheshimiwa Rais na tutapata matokeo, tutakuwa tumetimiza mchango wetu kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini labda makofi haya ni kwa sababu ya kuwezesha mapumziko ya nusu saa asubuhi. Lakini naomba nianze na hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuomba radhi na ni uungwana kwa Mheshimiwa Spika, kwa Bunge na Wabunge wote kwamba asubuhi kutokana na wingi na uzito wa hoja zilizotoka jana, asubuhi tuliamkia kwenye kuandaa majibu tukiamini kuna uwezekano tukamaliza mchana na kosa tulilofanya tulichojifunza ni kutabiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutabiri kwamba maswali huwa yanaisha saa nne na dakika 10 au 15 na utabiri huo umetokana na uzoefu wetu tu wa hapa kwamba dakika tano mpaka pale nimeshaingia. (Makofi)

Kwa hiyo, kumbe leo yameisha kabla ya saa nne, kwa hiyo, tunaingia tunapishana na msafara hapa wote na Naibu Waziri, tukatamani kuingia chini ya viti, lakini tunashukuru kwa uelewa wa Bunge na Waheshimiwa Wabunge tumejifunza. Kila jambo lina elimu, kuanzia leo hatutatabiri tena maswali yanachukua muda gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa shukrani, shukrani nyingi sana kwa Waheshimiwa Wabunge kwa kweli tumepata michango mingi na mizuri na yenye tija sana, sana, sana na imetusaidia sana na wataalam wetu kwa kweli wa Wizara nzima mmefanya wachemshe mbongo zao sana katika kutafuta majibu. Kwa hiyo, quality, ubora wa michango ya Waheshimiwa Wabunge kwenye Wizara yetu ulikuwa kiwango cha juu sana, sana, sana. Kwa hiyo, sisi tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pia kwa pongezi nyingi ambazo mmezitoa na kwa kweli hatukuzitegemea kwa sababu kuna mambo mengi yalikuwa yanapitapita kuhusu bajeti ya Wizara yetu, lakini sisi tulikaa kimya, tukawa tunafanya kazi, kila akija Mbunge tunampa msaada, tunajaribu ku-engage, tunajaribu kutoa taarifa na naamini kwamba kutokana na hayo kazi mmeiona na pongezi tunazipokea na pongezi ni deni. Kwa hiyo, tutaendelea kuhakikisha kwamba yale ambayo tumeyaahidi, tutayafanya na sisi tunaahidi ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa mchango wake ambao umesaidia kueleza baadhi ya mambo. Sasa michango ni mingi, ni zaidi ya 50 na ningependa kuwataja Waheshimiwa Wabunge wote na nataka kuahidi kwamba kwa yale ambayo sitayafikia tutawajibu kwa maandishi kabla ya Bunge hili la Bajeti kuahirishwa ili kila mmoja apate majibu ya yale ambayo tumeyaeleza. Nitajaribu kujibu kwa ujumla na nitarajibu kupitia michango ambayo imetolewa kwa Mbunge mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa masuala ya jumla ambayo nadhani ni muhimu nikayazungumza la kwanza ni hili la TPDC kushiriki kwenye biashara ya mafuta. Kwa sababu nadhani hili ni kubwa na la kisera na lazima tulitolee kauli na msimamo.

Kwanza ili uamue kwamba taasisi gani inafanya shughuli gani, lazima urudi nyuma uangalie imeundwa kwa mamlaka gani, kwa instrument gani na imepewa kazi gani ilipokuwa inaundwa yenyewe kwa sheria yake na sheria mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukienda kwenye sheria kubwa kabisa tuliitunga hapa ya Petroleum Act ya mwaka 2015. Sheria ile ina i-define TPDC kwamba ni National Oil Company, ni Kampuni ya Mafuta ya Taifa na imepewa kazi gani mle? Imepewa kazi nyingi, lakini moja ya kazi mle ni kwamba itashiriki katika mnyororo mzima wa biashara ya mafuta na gesi. Tunaposema mnyororo mzima, maana yake kuanzia utafiti, utafutaji, uendelezaji na uuzaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni muhimu tukayajua pia matakwa ya sheria kuhusu hili jambo, acha tu mambo mengine ya kibiashara lakini matakwa ya sheria kuhusu hii taasisi yetu. Lakini sisi imani yetu ni kwamba kushiriki kwenye mkondo wa juu kwa maana kutafuta na kuchimba siyo mutually exclusive na kuuza huku chini, unaweza kufanya vyote na vyote vikawa sahihi. Sisi tunayo mifano ya National Oil Companies za nchi nyingi na baadhi ya hizi tuna ushirikiano nazo. Mimi nilipata bahati ya kusafiri na Mkurugenzi wa TPDC kwenda kumtambulisha na kutambulishana kwenye National Oil Companies za nchi rafiki na nyingine tumeingia nazo makubaliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulienda Abu Dhabi National Oil Company kubwa sana, hii kampuni ina visima vya kuchimba, lakini wana-training wanauza rejareja na sisi kampuni tunayoshirikiana nayo ukisikia TPDC imeshinda tender, imenunua mafuta haya yaliyochakatwa kutoka Abu Dhabi National Oil Company ambayo ina mafuta, ina visima lakini pia inauza. Kuna kampuni inaitwa Sonatrach National Oil Company ya Algeria kubwa, ina visima, ina ma-refinery lakini inauza mafuta pia rejareja. Kuna nyingine inaitwa Sonangol ya Angola. Vilevile naweza nikataja kuna Aramco ya Saudi Arabia kama alivyosema ndugu yangu Mheshimiwa King.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sasa lazima tuliweke sawa, sisi kama Serikali tutaendelea kuiunga mkono TPDC na kuiwezesha ifanye kazi zake katika mnyororo mzima wa biashara ya mafuta na gesi. Lakini pia tukumbuke hili jambo ni kubwa la kimkakati, huwezi kuliacha. Sisi tulienda vitani, mzee wangu Kepteni George Mkuchika anafahamu, tulienda sisi na majeshi ya Idd Amin. Nchi zote na wauzaji wote wa mafuta walikataa ku-supply mafuta, nani alipeleka mafuta mstari wa mbele? Ni TPDC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pale kwenye ofisi zetu kuna nishani imesainiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Nishani wamepewa TPDC kutunukiwa na Mwalimu kwa kuhudumia nchi katika kipindi cha vita. (Makofi)

Kwa hiyo, kuna baadhi ya mambo hauwezi ukayaacha, ukaweka mkono wa Serikali na moja wapo ni mafuta. Hata hizo nchi tunazoziita za mabepari na nini kwenye haya mambo yaziondoi mkono zipo kwa sababu ni suala la usalama wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa hapa katikati kidogo tulilegea legea lakini tumerudi kwa nguvu kabisa kuiwezesha TPDC liwe shirika kubwa la mafuta ya Taifa na la kimkakati na liweze kufanya hii shughuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na pale kwenye TPDC kuna idara mbalimbali, kuna idara ya exploration wao wataendelea nao. Lakini kuna directorate/ Kurugenzi ya Oil and Gas Business ndiyo wanafanya hii shughuli. Kwa hiyo, idara hii wanaendelea, idara ile wanaendelea na shughuli nyingine wala haina mgogoro. Kwa hiyo, nisingependa hili likawa ni jambo ambalo likaaminika hapa na sisi tukalichukua. Kwa hiyo, hilo nilitaka niliseme kama jambo kubwa la kisera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni hili suala la kukatikakatika kwa umeme, amelizungumza Naibu Waziri na nataka niseme kwamba ipo miradi kuna package, labda niseme wote mnafahamu, sisi tulivyopewa nafasi hii na hapa Bungeni ikajitokeza hoja ikiwemo tuunde tume ya kusema kwa nini Waziri Makamba ameingia na umeme unakatikakatika sana. Ikawa ni kama jambo msukumiwa la mtu. Lakini sisi tukafanya utafiti na timu pale TANESCO, maana yake kulikuwa na maneno hujuma, hujuma, Hapana, siyo hujuma, mimi nilikuwa siamini kabisa kama watumishi wa Serikali na wa TANESCO wanaweza wakaihujumu nchi yao, kabisa hilo halipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tukagundua kwamba kuna baadhi ya maeneo na Wabunge ni mashahidi mmesema kuna baadhi ya line ni ndefu sana na zimewekwa kipindi kirefu kabla matumizi hayajapanuka na ni dhahiri kabisa hayatoshelezi. Kwa hiyo, tukafanya utafiti kila eneo ni karibu nchi nzima kuna vituo vidogo, kuna nyaya ndogo, nyembamba, kuna nyaya zingine zina-serve watu wengi, kuna transfoma nyingine zinahudumia wateja wengi zaidi kuliko uwezo na tukatengeneza package ya miradi inaitwa National Grid Stabilization Project ambayo ukiiweka thamani yake ni shilingi trilioni nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa safari hii tumebarikiwa, tumepewa shilingi bilioni 500. Nafahamu nimesikia suala la Mheshimiwa Kimei kwamba itaisha lini kwa sababu bilioni 500 ukilinganisha na trilioni nne na hapa ni under investment tuna-cover vitu ambavyo havikuwekezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba hatutategemea peke yake pesa hizi za bajeti kila mwaka katika kutafuta rasilimali za kurekebisha hali ya umeme. Zipo njia nyingi ambazo tunazifanya za kutafuta fedha ikiwemo hii ambayo tuliisema kwamba tukirekebisha vitabu vya TANESCO na Serikali ikafuta au ikachukua nusu ya deni; TANESCO itakuwa na uwezo wa kifedha wa kwenda kutafuta resources na kufanya hii miradi ambayo iko kwenye grid stabilization bila haja ya kuja hapa Bungeni mara kwa mara, kwa hiyo, hilo tunaendelea nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la kisera ambalo napenda kulizungumza hapa ni suala ambalo limezungumzwa kidogo kwa kirefu, ni hili suala la strategic reserve ya mafuta na amelizungumza Mheshimiwa Mwijage, Kamati imelizungumza, Mheshimiwa Kimei pia amelizungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa labda niweke vizuri, hifadhi ya mafuta ya kimkakati ni nyenzo ya usalama wa Taifa vilevile. Sisi hapa sheria zetu zinahitaji kwamba kwa wakati wowote hapa nchini mtu mwenye maghala ya mafuta au kituo cha mafuta awe na mafuta ya siku 15 za mbele kwa sababu ya dharura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tayari katika hiyo sheria, hiyo kanuni kuna element za kutaka kujikinga, kuwa na hifadhi nchini incase kuna dharura. Sasa sisi tumeweka siku 15 kwa sababu tu ya uwezo, uwezo wa hifadhi, uwezo wa mafuta na kadhalika. Kuna nchi nyingine zinahitaji siku 90, kuna nchi nyingine mpaka miezi sita kwamba at any given time nchi iwe na mafuta ndani ya nchi ya kutosheleza miezi sita, sisi tumeweka siku 15 zinatosha. Sasa ikitokea dharura ya siku ya zaidi ya siku 15 maana yake ni kwamba hamna mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tumeamua safari hii tufanye mambo ambayo yatatupeleka zaidi ya siku 15. Sasa mambo yenyewe ni yapi? Hifadhi ya kimkakati ya mafuta ya Taifa siyo lazima iwe ni physical kwamba mmechimba mashimo au matenki kuna mafuta pale yanasubiri tu dharura. Ukifanya hiyo, hiyo ni dead capital na mafuta pia yenyewe yanapungua ubora kadri yanavyokaa. Kwa hiyo, tunaposema hifadhi ya kimkakati ya mafuta hatuna maana tununue mafuta tuyaweke kwenye matenki, tusubiri dharura, hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna instruments nyingi za kuwa na petroleum strategic reserve na mojawapo ni aliyosema Mzee Kimei. Kikubwa ni kwamba at any given time ndani ya nchi either kupitia instrument mojawapo ni kuifanya nchi yetu iwe kituo kikubwa cha biashara ya mafuta, yaani nchi zote za ukanda huu ziwe zinanunua mafuta hapa, zinapitishia hapa, pana matenki hapa pia iwe trading hub, kwamba kama upo nchi nyingine unapiga simu kwamba nataka kununua mafuta chapchap basi unaambiwa Tanzania kuna tani 200,000 unaweza kuzipata haraka haraka na zile zinarudishwa haraka haraka. Hiyo ndiyo strategic reserve kwamba unayo at any given time, siyo ipo imelala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa tunachosema ni kwamba tutatumia na tutaleta hapa Bungeni, tutatumia baadhi ya hizi instruments za kisasa na za kibiashara za kuwa na mafuta mengi ya kutosha hapa nchini ikiwemo kuibadilisha Tanzania iwe kituo kikubwa cha mafuta katika ukanda huu. Kwa hiyo, hili ni jambo la kisera nataka niliweke, kwa sababu ukisema pesa, ukiwa na cash kwamba mimi nimeweka pembeni cash nikipata dharura niwe na uwezo wa kuagiza mafuta, saa nyingine unaweza kuwa na pesa za kutosha tu lakini physical huwezi kuyaleta mafuta hapa nchini. Kwa hiyo, lazima uwe na namna ambayo mafuta yanakuwa traded hapa hapa nchini. Kwa hiyo, hiyo tutaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine la kisera ni suala la umeme kwa ujumla. Malengo yetu ya kufikia megawati 5,000, tunafikaje, mahitaji ya nchi tunayajuaje, tunayapangaje, umeme wa aina gani, tunaufikishaje kwa watumiaji. Sasa moja ya vielelezo vya maendeleo ya nchi ni moja ni alilosema Profesa Muhongo per capital consumption ya energy.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyingine ni aina ya nishati watu wanayotumia, nyingine ni idadi ya watu wanaofikiwa na nishati hiyo na mwisho ni nishati hiyo inatumika wapi. Hiyo ndiyo energy profile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia nchi yetu aina ya nishati inayoongoza kwa matumizi siyo mafuta, siyo umeme, siyo gesi ni nishati inaitwa biomass. Kuni, mkaa, pumba, mavi ya ng’ombe na kadhalika. Asilimia zaidi ya watu 80 ya Watanzania ukichukua unit ya energy, magari yote yanayosafiri, mitambo yote inayozalisha umeme bado kiwango cha nishati kinachotumika ni kidogo kuliko kuni, mkaa, pumba. Sasa hiyo peke yake proportion ya biomass consumption inaelekeza kiwango cha maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa maendeleo yanapatikana mnapoondoka kwenye biomass na kuingia kwenye commercial traded modern cleaner energy, kwa sababu biomass moja ya sifa yake kwa mwaka hapa watu 22,000 wanakufa kwa kuvuta moshi wa kuni na mkaa watu 22,000, hizo ni statistic za Wizara ya Afya. Kwa hiyo, kwa kadri unavyoenda kwenye nishati safi ndivyo ambavyo unaokoa watu wako na unaingia kwenye uchumi wa kisasa. Sasa hiyo ya kwanza aina ya nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili je, nishati ya hapa Tanzania inatumika zaidi wapi kwenye usafirishaji, kwenye viwanda, majumbani? Ukitizama profile ya nishati hapa nchini haitumiki viwandani, inatumika majumbani na majumbani inatumika wapi. Je, kupoza vichwaji? Je, kupoza hewa? inatumika kupika. Kwa hiyo, utaona kwamba kwa nchi yetu kama wewe ni Waziri wa Nishati haujajielekeza kwenye nishati ya kupikia haujafanya kazi yako, kwa sababu ndipo ambapo consumption kumbwa ya energy ilipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunataka kwenda kwenye maendeleo ya viwanda, tunahitaji umeme zaidi, nami nakubaliana kabisa kwamba per capital energy consumption yaani kiwango cha nishati kinachosomeka kwa mtu lazima kipande, lakini hiyo ni function ya unazalisha kiasi gani; Pili je, una uwezo wa kuusafirisha huo umeme kwa hao watumiaji; Tatu je, wana-appliances za kutosha za kutumia umeme mwingi; na mwisho je, una viwanda vya kutosha kutumia umeme wa kutosha? Lakini ni yai na kuku kipi kimeanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutazalisha umeme mwingi tumeongea na wenzetu wa TANESCO, tunataka sisi kama tutapata dhambi, dhambi yetu iwe kuwa na umeme mwingi kuliko unaohitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuweze kuusambaza na kuupeleka kila mahala katika nchi hii, ndiyo maana utaona bajeti yetu hii ya safari hii ambayo sio mwisho ni mwanzo wa safari inatupeleka kwenye kuzalisha umeme mwingi lakini mtaona miradi mingi ya usafirishaji na mradi wa usambazaji ni hii ya vijijini. Kwa hiyo jambo la kisera sisi la kwetu ni siku zote kuendelea kuzalisha umeme mwingi wa kuwafikia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri tuliyonayo sisi katika ukanda huu tuna natural resource base ya kuzalisha umeme kuliko nchi nyingi katika uwanda huu ukiondoa Congo. Tunayo makaa ya mawe, gesi, jua, upepo na tunayo maporomoko ya maji. Kwa hiyo, ukilinganisha sisi leo tulikuwa tunapiga hesabu uki-exhaust resource base yote tuliyokuwa nayo sasa hivi tuna uwezo hata wa kufika hata megawatt 60,000 hatuzihitaji sasa lakini ndiyo safari hiyo tunayoelekea. Sasa nilitaka kusema kisera huo ndiyo mwendo na mwendo wa haraka na hatutasita kukimbia kwenye kupata umeme mwingi kiasi kikubwa, sasa hili nilitaka nisema jingine la kisera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Symbion ambalo alilizungumza Halima Mdee na suala la Mwalimu Nyerere na suala la TANESCO kwa ujumla. Sasa nianze na suala la Symbion sasa hili ni muhimu niliseme hapa Bungeni ili kuliweka vizuri kwa sababu limekuwa linasemwasemwa...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri una dakika Kumi.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nahitaji zaidi lakini nashukuru. Suala la Symbion limekuwa linasemwa sana, nataka kulisema kama ifuatavyo na hili litaendana na Mwalimu Nyerere ambalo nitalieleza. Suala la Symbion tunaweza tukarudi sana lakini nianzie 2011 ambapo TANESCO iliingia kwenye mkataba wa muda na kampuni hii Symbion ambayo ilikuwa na mitambo pale, ilikuwa mitambo ipo pale imekaa huko nyuma kulikuwa na mambo mengine kulikuwa na shida ya umeme wakaingia mkataba wa muda wa miaka miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkataba ukaisha 2013 wakaingia mwingine wa muda mpaka Septemba 2014, EWURA wakaandikia barua TANESCO kwamba hii mikataba ya muda mfupi mfupi ina gharama, TANESCO wakachukua ushauri wa EWURA wakaingia mkataba wa muda mrefu kati ya TANESCO, Symbion na muda mredu kati ya TANESCO na symbion Julai 2015. Septemba mwaka huohuo EWURA ikapitisha huo mkataba na mwezi Disemba Mwanasheria Mkuu naye akaupitisha, Tarehe 10 Disemba, 2015 Mkataba ukasainiwa lakini siku hiyohiyo ukaitishwa na baada ya hapo Tarehe 24 mwezi Mei mwaka 2016 mkataba ule ukavunjwa rasmi Machi 27, Symbion akaenda kwenye Mahakama ya Kimataifa ICC kudai fidia ya dola za Kimarekani Milioni 566 kwa kuvunjwa mkataba isivyo kufuata utaratibu na hasara ambayo itapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye shareholders wa Symbion wakaenda kudai Dola Bilioni Moja kutokana na kuvunjwa kwa industrial protection treat, tukawa tunadaiwa Dola Bilioni Moja na Nusu kutokana kwenye huo mkataba, mashauriano yakafanyika baadaye ikakubalika kwamba tuzungumze nje ya court na mazungumzo hayo yalikubalika Julai 28 na Februari 2021 makubaliano yakafikiwa, yalikuwa na sehemu tatu, Serikali TANESCO kulipa zile bilioni 300 na aliyosema Mheshimiwa Mdee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ilikuwa baada ya Serikali kulipa TANESCO kuchukua ule mtambo wa megawatt 112 kwa sababu ile ndiyo kisehemu kinaachwa, kukawa na ratiba ya kulipa hayo malipo la sivyo inarudi kwenye Mahakama. Sasa mwezi Agosti malipo yakafanyika kulingana Deed of Settlement ambayo Serikali ilisaini ili kuokoa adhabu kubwa ambayo tulikuwa tunaelekea kushindwa na mwezi Oktoba TANESCO ikauchukua mtambo, sasa kuanzia mwezi Novemba mtambo ukaanza kuzalisha umeme na tangu umeanza kuzalisha umeme mwezi Novemba mpaka sasa umezalisha unit hapa ziko nyingi ninazoweza kuzitaja, TANESCO imezalisha umeme na kuuza kwa faida, kwa hiyo ukipiga hesabu thamani ya mtambo wa megawatt 112 na mauzo ya umeme yanayopatikana katika mtambo ule basi unaweza kujua kama hayo makubaliano yalikuwa na tija, lakini sisi tunaamini kwamba Serikali kupitia Wanasheria na waliamini kabisa kwamba ni jambo ambalo lilipaswa kuiepushia Serikali hasara kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huo ndiyo ukweli kama unaweza kuutafsiri unavyotaka lakini mwisho wake maamuzi yalichukuliwa na Wanasheria wa nchi yetu walioangalia maslahi mapana ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mradi wa Bwawa la Julius Nyerere, sisi tuna mkataba mradi ule unaendeshwa kwa mkataba, mkataba unatoa haki na wajibu kwa kila upande, mkataba umeweka utaratibu wa kushughulikia kutofautiana, mkataba unatoa adhabu na sanctions mbalimbali, muda wa mkataba haujaisha, nasi tusingependa ku-litigate contractual matters kati ya two parties kwenye contract ambayo its operational hapa ndani ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mkataba huo unaendelea zitakapofika ratiba ambazo zimepangwa basi zitafika. Je, mradi utachelewa ndiyo mradi utachelewa kwa miaka miwili. Je, implication ya kuchelewa ipoje ipo ndani ya mkataba. Sisi kwetu mkataba uishe ukiwa bora na usalama mradi na sisi hatuoni kuchelewa kwa mradi wa Julius Nyerere kama ni disasters, mradi hapa wa Kidatu umejengwa miaka mitano, Kihansi miaka minne, Mtera miaka minne, Pangani miaka mitano, duniani kote miradi hii inapita ratiba, sisi focus yetu uishe kwa ubora na viwango na malengo yake yatimie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hasa naomba nitumie muda mchache uliobaki harakaharaka kumaliza na ndugu zangu wa Kigoma. Grid naomba Mzee Bidyanguze, Mama yangu Samizi, Kaka yangu hapa Kirumbe na wananchi wa Kigoma na Wazee wangu wa kule Buhigwe wote mnafahamu mimi ni wa Kigoma lakini siyo sababu ya kuweka grid. Kwa hiyo nafahamu ipo miradi minne ya kupeleka grid Kigoma. Katika miradi hiyo minne, miradi miwili Wakandarasi wapo site, mmoja anaitwa TATA anapeleka wa Kv 400 kutoka Nyakanazi mpaka Kigoma tumemlipa yupo site. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkandarasi wa pili yupo site anaitwa Sinotech anautoa Nyakanazi - Kakonko mpaka Kibondo tunayo line, kwa hiyo Kibondo – Kasulu - Buhigwe - Kigoma hii inaisha Oktoba, hii siyo story wako site. Kwa hiyo tunaposema grid inakuja Kigoma kabla ya Oktoba tunamaanisha hivyo. Waheshimiwa Wabunge nimalize kwa kusema Mzee wangu Salum nimekusikia mchango wako tumeuchukua, Mheshimiwa Mwakasaka vijiji vyako tumevichukuwa, Mheshimiwa Zedi, Mheshimiwa Jesca Kishoa tutakujibu kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shanif Mansoor, Mzee Usi Salum Pondeza, Mheshimiwa Lucy kutoka Simiyu tumetenga Milioni 725 kwenye mradi ule wa kupeleka umeme Bariadi, kwa sababu ndiyo kazi za kuanzia ikiwemo kulipa fidia, tukishalipa fidia na kumaliza ile EIA pesa Bilioni 65 zipo za kupeleka umeme wa grid Bariadi. Mheshimiwa Vuma nimeshajibu kuhusu grid na kukatika kwa umeme tumejibu, Mheshimiwa Makoa ndugu yangu vijiji vyako Kondoa Mjini na hapa siyo mbali, Mheshimiwa Monni nitakuja Chemba siyo mbali na Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava suala la mafuta tutakujibu kwa maandishi na umeme kukatikakatika tumejibu. Mheshimiwa Gulamali Bwawa la Mwalimu Nyerere hongera tumezipokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la hii Tume tuliyoiunda ya kwenda kuchunguza, labda niseme tu kwamba samahani tulipata shida moja, kwamba kama TANESCO na kama Wizara, tunaposema kwamba bei ya kuunganisha itokane na nguvu ya kiuchumi ya wahusika ambayo assumption ilikuwa ni aina ya settlement wanazokaa, kwamba watu wa mjini wana nguvu za kiuchumi wanaweza kulipa zaidi, watu wa vijiji tuwasaidie walipe chini. Sasa problem tuliyoipata ni hiyo katika miji kuna watu pembezoni mwa miji ambao pamoja na kwamba jiografia imewaweka ndani ya mji lakini hali yao inafanana na vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na option mbili, either kutengeneza a general rule ambayo itakuwa applicable kwa maeneo ya aina hiyo, jambo ambalo ni gumu, pili ni sisi kwenda physically wenyewe kuuchukua mtaa kwa mtaa inayofanana kama kijiji. Nadhani kwa hoja kama itachukuwa muda nadhani ni njia salama zaidi itakayo-target wahusika moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tunaomba mkubali hii na kama tulivyosema kwenye hotuba yetu tutawashirikisha katika hii, watu wetu mtawaona watakuja huko na tutafanya kazi.

Meshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Vita suala la kupeleka umeme kwenye hizi sehemu za huduma tumelipokea, kwenye bajeti tunao mradi wa kupeleka umeme katika mashule vituo vya maji na zahanati. Mheshimiwa Festo nimekuelewa sana vizuri sana kuhusu mchango wako ambao umetokana na experience yako ya kutembelea kiwanda cha kule ulipoenda, kuhusu Lumakali na Luhuji naomba niseme kwamba tumepata watu ambao wana-interest ya kuwekeza. Zile hela ulizoziona Bilioni Nane ni za kazi za awali kuhuisha ile feasibility study lakini tunakuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la GGM ambalo limezungumza na Mheshimiwa Musukuma nadhani na wewe na mwingine, pale kuna confusion, tumeingia nao mktaba nao mwezi Novemba tuwapelekee umeme, sasa ile substation inayoonekana pale Geita Mjini siyo yenyewe ya kupokelea umeme wa GGM. Tulikubaliana sisi tutaupeleka mpaka getini wao watajenga substation ndani, kwa hiyo kuna substation inayojengwa ndani ya mgodi ambayo inaisha mwezi Oktaba kwa mujibu wa makubaliano yetu, kwa hiyo bado tutapeleka umeme GGM na ile sheria uliyosema ya hovyo ya kwamba ukizalisha umeme huu, lazima tutaipitia kwa hakika kabisa ili kuwezesha wawekezaji wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Deo Mwanyika, suala la Mapembasi tutalimaliza na la Masista pia tutalimaliza. Mheshimiwa Getere mambo mengine uliyosema umepitisha kidogo lakini tunapokea pongezi. Hiyo Tume itakuja nashukuru kwamba umeona mambo yanaenda vizuri. Mzee Magessa naomba tisheti uivai ya vitongoji kwa sababu siyo tu tumeanza lakini dhamira ya kupeleka umeme kwenye vitongoji ipo kwenye bajeti yetu tunazo Shilingi Bilioni 140 za maandalizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, migodini mtaleta lini? Mkitazama kwenye bajeti yetu ya sasa tumetenga Shilingi Bilioni 20 kupeleka umeme migodini, viwandani na kwenye maeneo ya uzalishaji wa kilimo, haijawahi kutokea na tutaendelea kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mzee wangu rafiki yangu Kamonga Ludewa tumekupata tumekusika, Mheshimiwa Mohamed Saidi Issa ile sheria geothermal tutaifanyia mabadiliko, Mheshimiwa Ighondo Abeid tutakuja pamoja kama ulivyosema katika vijiji Tisa kuwasha pale Singida, Mheshimiwa Shabiby suala la bili la KVA naomba sana kwa ridhaa yako tuchukue haya makaratasi yako tuende pamoja TANESCO tukalitazame kama ni suala la mahsusu kama suala la jumla tutalifanyia kazi lakini suala la mafuta hizo taarifa ulizonazo za kuhusu bei zinavyopigwa tuko tayari kuzipokea, tuko tayari kuzifanyia kazi, wewe tuletee kwa pamoja ukitaka unaweza kuja na mtu mwingine ambae atakuwa shahidi wako namna tunavyolishughulikia hilo jambo kama huna imani na uwezo wetu wa kushughulikia hilo jambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Nusrat kuhusu Singida kuna miradi mitatu, katika hiyo uko mradi wa Manyoni, mradi wa Singida pale DC na Ikungi yote hiyo ipo katika uelekeo wa kutekelezwa. Manyoni tayari wako Masdar kampuni ya UAE kubwa kabisa ya renewable huu mwingine ipo kampuni ya upepo ambayo imepata zabuni na iko kwenye majadiliano na kampuni, lakini sasa muhimu kujua ni umeme unapozalishwa pale Singida siyo kwamba ni wa Singida ni kwa sababu tu Singida ipo kwenye grid utaenda pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la hospitali hazijaunganishwa ukitazama kwenye bajeti yetu utaona kwamba katika mwaka huu tuna hospitali zaidi na vituo vya afya zahanati zaidi ya 114 ambazo tumezipelekea umeme mahsusi na hapa ndipo tunapoanza, tunaongea na wenzetu katika TAMISEMI na kwingineko kwamba tunapopanga hii miradi tupange pia na component ya umeme, kwa sababu saa nyingine tunasahau unaweka kule halafu kumbe umeme hakuna kwa hiyo REA leteni, kwa hiyo kwenye cost ya miradi tuta-coordinate na wenzetu ili cost ya mradi wote iwe pia na gharama ya kupeleka umeme pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mhagama nimekupata, Mzee George Malima, REA ipo center ni kweli, Mpwawa na bei ya kuunganisha nimezungumza, Mheshimiwa George Mwenisongole suala la wakandarasi amelizungumza Naibu Waziri, suala la Mkuu wa Mkoa nadhani mimi na wewe tutalizungumza pamoja na Waziri wa TAMISEMI kuliweka vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dada yangu Mariam Mtanda megawati 300 za Mtwara ambayo pia amezizungumza Mheshimiwa Mwambe megawati 300 za Mtwara pesa imepatikana na siyo tu ya megawati 300 lakini pia na waya wa kuleta mpaka Somangafungu, Wajapan watatuchangia.

Mheshimiwa Francis Isack, Mkalama nimechukua, tutakujibu kwa maandishi; ndugu yangu Mheshimiwa Hassan Kungu kutoka Tunduru naelewa kabisa ile KV 33 kutoka Songea ni ndefu bila shaka na katika ule Mradi wa Grid Stabilization ipo ya ku-upgrade ule waya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mjomba wangu Mheshimiwa Rweikiza kazi bado sana; ni kweli na umeme unazimika sana tumelizungumza, Mheshimiwa Florence Samizi, gridi nimezungumza, Malagarasi pia tunaanza; Mheshimiwa Bidyanguze pesa ipo tumamazila evaluation, ndani ya mwezi tuna-award Mkandarasi aanze ujenzi pale.

Kuhusu madeni makubwa TANESCO labda niweke tu vizuri status ya TANESCO, TANESCO assets value yake ni trilioni 17, madeni yake ni trilioni tatu, katika hayo madeni trilioni mbili ni madeni ya Serikali ya on landing na trilioni moja ni watoaji huduma ikiwemo TPDC, PAET na kadhalika. Kwa hiyo, ni vizuri hizi takwimu za financial position ya TANESCO zikajulikana kwa sababu saa nyingine tunachanganya, ukisema TANESCO ina deni la trilioni 13 si kweli ni ina asset ya trilioni 13.

Mheshimiwa Anastazia Wambura la megawati 300 nimelizungumzia, Mzee Mulugo, lile suala la helium tumelizungumza ofisini, ni la ndani ya Serikali tutaliweka vizuri; Mzee Felix wa Buhigwe nimejibu na mengine tutajibu; Mheshimiwa Issa Mchungahela, umelihutubia Taifa, hotuba yako imepokelewa basi tutayafanyia kazi ambayo umeyasema. (Makofi)

Mzee Almas nimeelewa sana kuhusu Msamvu na ni critical na kuungua mara mbili ndani ya miezi sita ni jambo ambalo inabidi lituinue, na mambo mengine hatuyasemi hapa, lakini kuna hatua tumechukua za kiusalama za kuuchunguza lakini pia na kuimarisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafutaji wa mafuta tumeongea kwenye bajeti tutaenda nao; Mheshimiwa Godwin Kunambi na Mheshiwa Vedasto tulizungumza kuhusu watu wanataka kuunganisha umeme, je, kwa nini tusiwakopeshe halafu wakalipa kidogo kidogo kwenye bili zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tumelitafakari na tunaendelea kulitafakari, tumepokea proposal mbalimbali na wachambuzi wa fedha wanafanya, challenge iliyopo ni kwamba vifaa vya kuunganisha vile vinaweza vikafika labda shilingi 200,000 au shilingi 300,000 lakini kasi ya kununua umeme ikawa ni shilingi 2,000 kwa mwezi au mtu ananunua LUKU anakaa nayo miezi sita, mnalazimika kutafutana, kutaka kung’oa, kukatiana umeme, mtu akiongeza tu umeme wake umeukata, kwa hiyo inaweza ikaleta ugomvi.

Kwa hiyo the debt collection component ya hii programu ni lazima tuiweke vizuri ili tusigombane na watu wetu kwa sababu kama mtu yuko nyuma ya deni akiweka LUKU tu maana yake imeliwa, sasa tutakuwa tunagombana na wateja. Lakini ni jambo ambalo tunalitafakari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti wa mafuta Mheshimiwa Mohamed Monni nimeshazungumza; Mheshimiwa Mama Stella Manyanya ile evacuation ya umeme kutoka Julius Nyerere nielezee kidogo tu, Julius Nyerere siyo mradi mmoja, siyo bwawa; kuna bwawa, kuna usafirishaji yote inaenda kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwambe kuhusu LNG, tutafanya na tunafanya na tumeanza bila shaka yoyote Bandari ya Mtwara na miundombinu ya Mtwara itatumika katika utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Mariam kuhusu teknolojia ya live wire na usalama kwenye LNG tumepokea; Mheshimiwa Kingu ahsante sana kwa shukrani, kuhusu tender iliyofutwa, tender hii safari hii ilisimamiwa na GPSA, GPSA iko chini ya mamlaka mengine na sisi tutakachofanya ni kufuatilia nini kilitokea, ila jambo ambalo ni la kweli kabisa ni kwamba fuel marking bado ni shida, haifanyiki kwa mtu yoyote wa mafuta atakwambia fuel marking haifanyiki kwa viwango vinavyohitajika na bado ni mtihani capacity ya TBS bado iko chini, tunaongea na wenzetu kuweza kuiinua. Kwa hiyo la tender tutalifuatilia halafu tutatoa taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mzee Bidyanguze, nimezungumzia la Malagarasi nashukuru na umeme utapatikana lini kwenye vitongoji tutaeleza kwenye siku zijazo; Mzee Kimei tumezungumza kuhusu densification inaendelea na kutafuta sources zingine kwa sababu umeme vijijini ndiyo densification yenyewe; ndugu yangu wa Mbinga kweli basi kwa kuchelewa basi tutafika na mimi ahadi yangu iko palepale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mwisho kabisa najua huwezi kuzungumza hapo ulipo ila Mfindi Kusini hatujaisahau kupeleka umeme katika sahanati, shule na sehemu za huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mengi na niseme tu kwamba nishukuru tena kwa michango kwa kweli mmetutia moyo sana, mmetupa nguvu na haya ambayo tumeyaweka kwenye kitabu chetu ni safari ni mwanzo wa safari siyo yote yataisha mwaka ujao wa fedha, tumeyaweka pale mengine ni endelevu kama mnavyojua yanaonekana ni masuala ya kuendelea. Lakini naomba niwashukuru sana kwa ushirikiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuzungumza na napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri aliyoitoa na kwa mipango mizuri ya Wizara.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika taasisi ambapo uongozi unafundishwa vizuri kwa nadharia na vitendo ni pamoja na jeshini na hii ni kote duniani, iwe West Point, Sandhurst au Monduli. Tangu nchi yetu ipate uhuru, viongozi wa Taifa hili tangu Baba wa Taifa mpaka Rais Magufuli wameenda jeshini kuchota katika kisima cha hazina ya uongozi iliyopo jeshini ili kusaidia kuongoza nchi yetu. Askari wetu wote walioombwa au walioteuliwa kutumikia nafasi za uongozi katika nchi na katika siasa kutoka jeshini wamefanya kazi nzuri na kubwa na mifano iko mingi, Jenerali Kimario, Jenerali Sarakikya, Jenerali Luhanga na wengineo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu katika hotuba ya Kambi ya Upinzani, ukurasa wa 12 kuna hoja imetolewa pale, kwamba ili kulinda na kusimamia maadili ya kazi ya jeshi, Wanajeshi wasihusishwe kabisa na kazi za siasa iwe wapo kazini au wamestaafu. Wanaendelea kusema kwamba kwa kuwateua kushika nafasi za siasa wanapostaafu, kunaweza kuwafanya wale wengine waliopo kazini kutozingatia maadili yao ya kazi na kuanza kujipendekeza kwa watawala. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ngazi kumi za uafisa jeshini, ngazi saba Rais ndiye anayepandisha vyeo. Kwa hiyo, kama kuna hoja ya kujipendekeza kwa Askari wetu, isingekuwa kwenye ngazi za siasa hata kule kule waliko jeshini kama tunaamini kwamba kwa weledi wao na mafunzo yao wametengenezwa na wamefundishwa katika hulka za kujipendekeza ingekuwa tunaiona kuanzia sasa kwa sababu bado Rais anapandisha vyeo jeshini. Kwa hiyo, nadhani kwamba ni kuwadhalilisha Askari na Maafisa wetu kwa kusema kwamba wanajipendekeza kwa watawala ili wapate nafasi.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi letu limewekwa chini ya mamlaka ya kiraia na sisi viongozi wa kiraia tunapigiwa saluti wakati mwingine na Askari. Leo wakati tunapitisha bajeti hii, wamekuwepo Askari na Maafisa wengi na wameshuhudia jinsi tunavyoendesha mambo yetu, nadhani baada ya kupitishwa bajeti hii na naamini itapita, tutakapokuwa tunarudi nyumbani kwetu tutafakari kama waliyoyaona tunayafanya Askari wetu leo hapa kama kweli watatupigia saluti huku ndani ya mioyo yao wakiwa hawaamini kama tunazistahili kama watakuwa wanakosea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu wa Spika, naomba nimalizie kwa kuwashukuru Askari wetu wote, Maafisa na wale wanaowaongoza kwa kuendelea kuifanyia kazi nzuri nchi yetu. Napenda kuwashukuru binafsi kwa kutuongoza na kufanya kazi vizuri. Napenda makusudi kabisa niwataje kwa sababu huwa hawatajwi hasa viongozi wale, Mkuu wa Majeshi yetu Jenerali Mwamunyange, ahsante sana. Mnadhimu Mkuu Lieutenant General Mabeyo, ahsante sana. Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Meja Jenerali Mwakibolwa ahsante sana. Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Wanamaji, Rogastian Laswai, ahsante sana. Mkuu wa JKT, Brigedia Jenerali Isamuhyo, ahsante sana. Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Anga, Brigedia Jenerali Ingram, ahsante sana. Mnastahili shukrani zetu sana kwa kazi nzuri mnayoifanya, kwa sacrifice mnayoichukua kulinda mipaka ya nchi yetu, kulinda amani ya nchi yetu na wakati mwingine maneno ambayo yanasemwa humu ndani ya kuwadhalilisha hamuyastahili na Watanzania wote wako nyuma yenu, ahsanteni sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 – Wizara ya Fedha na Mipango
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuchangia. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara; kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kuandaa bajeti hii. Nawapongeza sana Wabunge wa CCM kwa kutimiza wajibu wao waliotumwa na wananchi wao kwa kutimiza sababu yao ya kuchaguliwa kwa kuingia Bungeni kufanya kazi waliyotumwa na wananchi na kueleza shida za wananchi wao mbele ya Serikali, nawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo kadhaa ambayo ningependa kuyazungumzia, la kwanza ni suala la VAT kwa Zanzibar na Bara. Kuna upotoshaji mkubwa sana kwamba hatua iliyochukuliwa na Serikali, hatua nzuri kabisa ya kuhakikisha kwamba bidhaa zinazozalishwa Tanzania Bara kwenda Zanzibar VAT inakusanywa Zanzibar; na bidhaa zinazozalishwa Zanzibar na kuletwa Tanzania Bara VAT inakusanywa Tanzania Bara. Kuna upotoshwaji mkubwa sana unaofanywa na wenzetu kule Zanzibar kwamba hatua hiyo inaiumiza Zanzibar, si kweli, ni kunyume chake. Hatua hii inainufaisha Zanzibar, hatua hii itawaumiza wale wadanganyifu wachache, waliokuwa wanatumia utaratibu huu kujipatia kipato ambacho sio halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ambalo ningependa kulizungumzia ni ahadi ya Chama cha Mapinduzi kwenye Ilani yetu kwamba kila kijiji kitapatiwa shilingi milioni 50 kwa ajili ya uwezeshaji, ukopeshaji wa wajasiliamali. Ahadi hii ya CCM ni hatua kubwa ya kimapinduzi ya kumuondoa Mtanzania katika lindi la umaskini. Mzunguko wa shilingi milioni 50 katika kijiji ni pesa nyingi sana zitakazoleta chachu ya maendeleo pale kijijini. Serikali katika mwaka huu wa fedha kama ambavyo mmeona, imetenga shilingi bilioni 59 kama kianzio, lakini zaidi ya hapo Serikali imeunda jopo la wataalam ambalo linatengeneza utaratibu madhubuti kabisa. Utaratibu utakaozingatia uzoefu wetu huko nyuma wa mifuko mbalimbali na mafanikio ya mifuko hiyo ili tuwe na utaratibu mzuri utakaohakikisha fedha hizi zinatumika kama zilivyopangwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni jambo kubwa linabidi lifanyike kwa umakini na umahiri mkubwa ili tusipoteze fursa hii adhimu katika kuwaokoa watu wetu. kwa hiyo utaratibu mzuri unaotengenezwa na Serikali utaletwa hapa Bungeni ili kabla ya kutumika na ninyi Waheshimiwa Wabunge muwe na mchango wenu katika aina ya utaratibu ambao Serikali itautumia na ikiwezekana kabisa aidha ni kwa kuleta Sheria mpya au kufanya mabadiliko ya Sheria katika Sheria ya Uwezeshaji sasa hivi. Ili fedha hizi ziwe katika msingi wa kisheria na ziweze kutumika vizuri kuliko mifuko mingine yote huko nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli kwamba zimetengwa shilingi bilioni 59, haina maana kwamba tutashindwa ndani ya miaka mitano kufanya vijiji vyote; tumeweka hizi ili tuanze na tujifunze na kadri tutakavyokuwa na utaratibu mzuri, kasi ya kupanga fedha nyingi zaidi ili tutimize ahadi hii kwa miaka mitano inakuwepo. Kwa hiyo napenda kuwahakikishiwa Waheshimiwa Wabunge na watanzania, kwamba hii ni ahadi ya CCM, hii ni ahadi ya Rais na itatimia bila shaka yoyote.
Naomba niseme kidogo jambo moja muhimu. Sisi Chama cha Mapinduzi tulipomteua Dkt. John Pombe Magufuli kuwa mgombea wetu, tulitoa statement duniani kwamba tunahitaji aina mpya ya nchi kutokana na aina ya kiongozi huyo. Kwetu sisi kumteua yeye tulitoa kauli duniani kwamba tunataka mabadiliko ya kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko ya kweli hayawezi kuletwa kwa hatua ndogo ndogo, mabadiliko ya kweli yanaletwa hatua kubwa na yanaletwa na uthubutu na uthubutu huo umeanza kujidhihirisha katika bajeti ya mwaka huu, tumethubutu kwamba tunaweza kukusanya shilingi trilioni 29.5; tumethubutu kwamba tunaweza kutenga asilimia 40 kati ya hizo kwa maendeleo. Unapothubutu jambo kubwa kuna watu watatia shaka, sisi wana CCM Serikali hii ni ya kwetu, Bunge hili ndio wengi, ilani ni ya kwetu, tusitetereke katika uthubutu wetu wa kukusanya shilingi bilioni 59 tumsaidie Rais tuisaidie nchi yetu kufikia malengo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa suala la hatua za kikodi hapo mbalimbali imetokea malalamiko kwamba kodi ni kubwa, kodi ni nyingi zitadhohofisha uwekezaji. Jambo hilo si la kweli kwa sababu utafiti unaonyesha mimi hapa ninayo ripoti inaitwa Tax incentive in a global perspective inasema kwamba; survey analysis shows that host country taxation and international investment incentives generally play only a limited role in determining the international pattern of FDI. Factors like market characteristics, relative production costs and resource availability explain most of the cross-country variation in FDI inflows. Transparency, simplicity, stability and certainty in the application of the tax law and in tax administration are often ranked by investors ahead of special tax incentives.
Suala siyo kiwango cha kodi, suala ni mfumo wa kodi. Kwa hiyo, miaka yote tumeaminishwa kwamba ukiweka kodi ndogo wanakuja, ukiweka kodi kubwa hawaji, dhana hiyo si ya kweli. Ukitengeneza mambo mengine vizuri zaidi ndiyo wanakuja ikiwemo uhakika wa mfumo wa kodi. Kwa hiyo, tusiwatishe wananchi na tusitishane hapa kwamba kiwango cha kodi tulichoweka kitafukuza wawekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ngoja nimalize kwa kusema kwamba Rais Magufuli tumempa usukani wa kuiongoza nchi yetu, lakini nchi hii ni yetu sote na sisi tunawajibu wa kumsaidia ili tufanikiwe. Rais Magufuli akifanikiwa, nchi yetu imefanikiwa sisi tusiwe kama watazamaji kwamba ngoja tumuone atafanyaje, sisi tuko naye kwenye basi hili tumsaidie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua tunazochukua nchi yetu ni sawasawa na gari nzuri aina ya benzi iliyoingia kwenye matope tunataka kuirudisha kwenye lami, hatua ya kuirudisha kwenye lami itakuwa na misukosuko, kuna wengine wataamua kushuka lakini tuendelee kuwa ndani ya gari hilo mpaka likae kwenye lami lifike safari. Maendeleo yanahitaji sacrifice, katika bajeti hii Wabunge sisi tume-sacrifice, tume-sacrifice kwa kukubali kukatwa kodi, kila mtu lazima a-sacrifice, wafanyabiashara, waendesha bodaboda, kila mmoja lazima a-sacrifice ili nchi yetu iende mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema mwaka 1961 wakati Rais Kennedy wa Marekani anaapishwa aliwaambia wa Marekani kwamba ask not what your country can do for you, but what you can do for your country. Ni wakati sasa kwa Watanzania wote kutokaa siku zote na kujiuliza nchi hii itanifanyia nini bali sisi tutaifanyia nini nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa na mimi kuchangia hoja hii ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Kamati na Mwenyekiti na Kamati nzima kwa kweli kwa ripoti nzuri waliyoiandika, kwa mapendekezo mazuri, lakini pia kwa ujumla kwa kazi nzuri wanayoifanya kuisadia Serikali wakati wote ambapo tumekuwa tunafanya nao. Kamati hii imesheheni wanamazingira, wanafahamu changamoto zilizopo na wamekuwa wanatusaidia vizuri sana katika kufanya kazi zetu. Nawapongeza na nawashukuru sana. (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge, kwanza tumepokea mapendekezo ya Kamati, ni mazuri na mimi nayaunga mkono, lakini pia tumesikia michango ya Wabunge kuhusu masuala ya mazingira. Wabunge wote waliochangia kuhusu eneo hili wamesema hali ya mazingira nchini ni mbaya na mimi nataka niseme kwamba hali ya mazingira nchini ni mbaya sana, si tu ni mbaya, ni mbaya sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maji katika nchi yetu ni rasilimali kubwa, ukitazama mito, vijito, mabwawa, chemichemi, kila mwaka unaopita tunapata changamoto ya upatikanaji wa maji, kwenye ardhi rutuba inapungua, matumizi yasiyozingatia kanuni za masingira, misitu inateketea, mvua hazitabiriki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka hapa tunakutana kupanga maendeleo na kupanga maendeleo na kupanga fedha za maendeleo. Ile shughuli za kupanga maendeleo na kupanga fedha za maendeleo itakuwa haina maana kabisa kama hatutazingatia umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwenye sekta zote. Ukitaja kilimo, hakiwezekani kuwa na manufaa kama hakizingatii mazingira. Afya, elimu, maji, utalii, hakuna sekta isiyoguswa na mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ya nchi yetu yana mahusiano moja kwa moja na hifadhi ya mazingira lakini pia hata uwezeshwaji wa wanawake (women empowerment) na yenyewe moja kwa moja ina uhusinano wa hifadhi ya mazingira. Tunapozungumza ukosekanaji wa maji unaotokana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi wanaoathirika zaidi ni akina mama. Tunapozungumza suala la nishati ya kupikia, wanaotumia muda mrefu kwenda kutafuta kuni na hata wakati mwingine kuingia katika mazingira hatarishi huko porini ni akina mama na ndiyo maana sikushangaa kwamba Wabunge waliochangia kwa sehemu kubwa kwenye mazingira ni akina mama, Mheshimiwa Leah Komanya, Mheshimiwa dada yangu mpendwa sana Hawa Bananga, Dkt. Christine Ishengoma, Mama Mwanne Mchemba kwa sababu ni jambo linalowagusa akina mama sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba tumepokea mapendekezo na tumeyakubali na tunapenda Bunge litusaidie kwa sababu Bunge ndilo linalogawa fedha, Bunge ndilo linaloamua fedha kiasi gani ziende katika maeneo gani. Waheshimiwa Wabunge, mkiamua ninyi kwamba Mfuko wa Mazingira katika mwaka ujao wa fedha uwe na shilingi bilioni 200 badala ya sifuri mnaweza kufanya hivyo. Sisi tulipanga katika bajeti iliyopita, tulijadiliana ndani ya Serikali lakini na hapa Bungeni kuhusu uwezekano wa mfuko wetu kupata vyanzo vya moja kwa moja kwenye tozo mbalimbali ili uweze kuwa na fedha nyingi zaidi ili mimi kama Waziri mwenye dhamana ya Mazingira nikipita kwenye majimbo nikiona unahitaji miche 10,000 niwe na uwezo wa kukupatia miche 10,000. Nikiona unahitaji kwa kupitia Mfuko wa Mazingira, vyanzo vya maji vitunzwe kwenye jimbo tuweze kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo napenda nirudishe changamoto hii kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba tunaelekea kwenye bajeti na kama kweli tunaamini mazingira ni muhimu basi pale tuoneshe kwa vitendo kwamba Mfuko wa Mazingira upate vyanzo vyake vya moja kwa moja kama ambavyo mfuko wa barabara unapata vyanzo moja kwa moja, kama ambavyo Mfuko wa Nishati unapata vyanzo moja kwa moja na mifuko mingineyo, mtakuwa mmetusaidia na mtakuwa mmeisaidia nchi yetu sana. Kwa hiyo ndugu zangu bila fedha hifadhi ya mazingira ni jukumu la moja kwa moja la msingi la Serikali. Sekta binafsi inaweza kushiriki kwenye hifadhi ya mazingira lakini hatuwezi kubinafsisha hifadhi ya mazingira. Lazima sisi kama Bunge tupange fedha ili zitumike huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu tatizo la mkaa. Tumeamua sisi kama Serikali kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kukabiliana na changamoto hii. Sasa hivi tutaleta mapendekezo; tozo kwenye kila gunia la mkaa ni shilingi 16,000 za TFS; labda Halmashauri inaweza na yenyewe inaweza ikacharge shilingi 2,000. Tunataka tuongeze kodi kwenye mkaa ili tuweze kupata fedha nyingi zaidi na tutapenda fedha hizo ziingie kwenye mfuko wa mazingira. Tungependa Wabunge mtusaidie tuamue na Waziri wa Fedha yuko na mazungumzo yanaendelea Serikalini; kwamba zile teknolojia ambazo zinasaidia uhifadhi wa mazingira basi zisamehewe kodi ili gesi iwe bei rahisi, majiko ya gesi yawe bei rahisi ili wananchi wa kawaida waweze kuyamudu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mradi wa maji Simiyu, Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza vizuri ila nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba moja ya nyenzo ambazo tumeamua kuzichukua kama Ofisi ya Makamu wa Rais ni kutumia hii mifuko mikubwa ya kifedha ya kimataifa kupata fedha kwa ajili ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi lakini fedha hizo kuziingiza kwenye miradi ya maendeleo. Kwa mfano, kwa uhakika kabisa Mkoa wa Simiyu utapata shilingi bilioni 200 kwa ajili ya upatikanaji wa maji kutokana na Mfuko wa Mazingira wa Dunia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kwenye maeneo yote yenye ukame kama Serikali tujenge hoja kwamba ukame ule unatokana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Kwa hiyo, fedha inazosaidiwa Tanzania kwenye kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi tuzipeleke kwenye maeneo kama hifadhi ya maji, kilimo cha umwagiliaji na kadhalika. Tukifanikiwa katika mwezi huu wa tatu unaokuja kupata fedha hizo shilingi bilioni 200 itafungua mlango wa kupata dola milioni 800 kwa ajili ya maji katika nchi yetu. Huu ni mradi ambao tunaufatilia kama Ofisi ya Makamu wa Rais na tutafanikiwa, tutakapofanikiwa basi wetu tutakuwa tumewapunguzia kero.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ukataji wa miti na kilimo cha kuhamahama, nimesikia nilipata nafasi ya kufanya ziara ya mikoa kumi katika nchi yetu na baada ya Bunge hili tutazunguka katika mikoa yote siyo tu kukagua hali ya uharibifu wa mazingira bali kuchukua hatua wakati ule ule tutakapoona kuna uharibifu wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwenye tumbaku Tabora, tumeamua sasa kupiga marufuku matumizi ya yale mabani ya zamani ya kienyeji ambayo yanatumia magogo mengi na kupelekea ukataji wa miti na misitu ya nchi yetu. Ningependa Bunge lako liwe ni Bunge la wanamazingira. Naomba tusaidiane sana, Waheshimiwa Wabunge mkiishika ajenda ya mazingira tutatoka, pamoja na kwamba inawezekana athari za uharibifu wa mazingira zisionekane papo kwa papo lakini madhara yake huko mbele yatakuwa maisha magumu sana kwa Watanzania. Kwa hiyo, tuna uwezo wa kuweka historia kama Bunge la kwanza lililoweka fedha nyingi zaidi kwenye hifadhi ya mazingira na kuyaokoa mazingira ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja hapa kila mwaka tunaomba fedha nyingi kwenye bajeti ya maji, lakini unaweza kuomba fedha na kujenga miundombinu ya maji kama hatukupanga fedha za kuhifadhi vyanzo vya maji tutakuwa tumepoteza fedha kwenye kujenga mabomba ya maji wakati kule maji yanakotoka hatujayahifadhi.
Kwa hiyo, katika shughuli zote ambazo tunazipanga katika Bunge hili mazingira ndiyo msingi wake na Serikali tunaishukuru sana Kamati kwamba jambo hili imeliona na inalishughulikia, tunategemea sasa spirit hii ya Kamati basi Bunge zima na yenyewe italichukua ili itakapofika wakati wa bajeti basi wote tuzungumze kwa kauli na sauti moja ili tuweze kuisaidia nchi yetu.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa fursa hii, naishukuru tena Kamati na ninawashukuru wote mliochangia kwenye hoja hii.
Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kuchangia hoja ya Waziri.
Kwanza, nianze kwa kutoa pongezi kubwa sana kwa hotuba nzuri na mipango mizuri iliyotolewa katika hotuba ya leo. Vilevile napenda kumpongeza Mheshimiwa Nape Nnauye, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri sana wanayoifanya katika majukumu waliyokabidhiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikubaliane na sehemu ya mchango iliyotolewa asubuhi hii na Mheshimiwa Zitto Kabwe, kwamba kijana akipewa majukumu na akafanya vizuri basi ni fahari kwa vijana, kauli hiyo ni sahihi kabisa. Pia naamini kwamba kijana akipewa majukumu anastahili kutiwa moyo, kuungwa mkono hasa na vijana wenzake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya mchango ulivyotoka asubuhi, ni kana kwamba Mheshimiwa Nape kazi hii amepewa miaka minne iliyopita na imeshamshinda na hana ubunifu. Aina ya mchango ule unakatisha tamaa, haumpi moyo Mheshimiwa Nape kama inavyostahili. Majukumu haya Mheshimiwa Nape amekabidhiwa takribani siku 160 zilizopita, kwa hiyo, bado kuna muda mrefu wa kufanya kazi na kuonesha ubunifu, na mimi sina shaka yoyote kabisa na uwezo wake wa kufanya kazi hii vizuri. Sikubaliani kabisa na dhana kwamba katika nchi hii mtu anayechukiwa zaidi ni Mheshimiwa Nape Nnauye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilipata bahati, Mheshimiwa Nape aliniomba nimsindikize kwenye Chuo Kikuu cha Dodoma ambapo kulikuwa na shughuli ya vijana; walikuwa wengi takribani 8,000 mpaka 10,000. Alipotambulishwa, nilliyoyaona hayaendani na kauli zinazosema kwamba hapendwi hapa Watanzania. Ushuhuda wa mambo hayo siyo maneno yangu tu, hata record ya shughuli hiyo ipo wazi na ilioneshwa. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama kuchangia hotuba hii, lakini hasa hasa kuzungumzia hotuba ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani hasa ukurasa wa 11. Niseme tu kwamba binafsi huwa naheshimu karibu kila mtu hapa Bungeni na sijawahi kuinua mdomo wangu au kauli yangu pale mtu anapotoa mchango wake. Kwa hiyo, nategemea heshima hiyo iwe accorded kwa Waheshimiwa Wabunge wote, kwamba kila mtu anapopewa nafasi ya kuzungumza, basi angalau kwa Kiingereza wanasema; “decorum.” Kwamba angalau kuwepo na decorum ya kumheshimu mwenzako amalize anachosema na fursa inapopatikana, kama hukubaliani naye, basi unaweza kusema hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 11 wa hotuba, imejengwa dhana hapa kwamba Chama cha Mapinduzi na Serikali ya Chama cha Mapinduzi na Mheshimiwa Rais anabagua wasanii. Katika vitu ambavyo viko mbali na ukweli, hiki ni namba moja. Linalozungumziwa hapa ni kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alialika baadhi ya wasanii na kuwabagua wengine. Kwa hiyo, wenzetu wanasema hicho ni kitendo cha Serikali, cha Rais kuwabagua wasanii ili awatumie kwa ajili ya maslahi ya kisiasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata bahati ya kuandaa hiyo shughuli inayozungumzwa na kushiriki kuiendesha. Katika shughuli ile Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwangu na kwa wenzangu kwamba angependa kutoa shukrani kwa makundi mbalimbali yaliyoshiriki kwenye kampeni ya CCM wakiwemo wasanii walioshiriki katika kampeni ya CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa uchaguzi kulikuwa na wasanii ambao walituunga mkono CCM na kuna wasanii ambao hawakutuunga mkono. Katika shughuli ile walialikwa wasanii, madereva, makundi mbalimbali; vijana wa IT pia walishiriki. Ilikuwa ni shughuli ya Mheshimiwa Rais kutoa shukrani kwa watu walioshiriki katika kampeni yake na kampeni ya CCM. Shughuli ile ya kushukuru watu imeendelea, haikuishia kwa makundi yale ambayo yalialikwa mwezi wa pili ambapo mimi nilishiriki, lakini pia viongozi wa CCM na viongozi wengine na kazi hiyo inaendelea.
Katika shughuli ile, masuala ya maslahi ya wasanii yalizungumzwa kwa mapana yake. Mheshimiwa Rais alielekeza hatua kadhaa za msingi za kuchukua na Mheshimiwa Waziri amezizungumza baadhi ya hatua hizo leo za kusaidia wasanii kujikwamua na changamoto zilizopo. Bahati nzuri sasa katika hatua zilizochukuliwa, katika utekelezaji wake zitawanufaisha wasanii wote waliotuunga mkono na ambao hawakutuunga mkono, walioshiriki shughuli ile na ambao hawakushiriki shughuli ile kwa sababu hatua zile hazibagui mtu, hazibagui wasanii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka nichangie, niweke record sahihi kwamba Mheshimiwa Rais wetu ni Rais wa watu wote na ni Rais wa wasanii wote. Serikali ya CCM ni Serikali ya watu wote, ni Serikali inayowaongoza na kuwaletea maendeleo hata wale ambao hawakutuunga mkono; kwa sababu sisi ndio tumekabidhiwa dhamana ya uongozi wa nchi na dhamana ya kuleta maendeleo ya nchi hii, na kazi hiyo tunaifanya na tutaifanya vizuri; na matokeo ya kazi hiyo yataonekana mwaka 2020 pale ambapo tutaongezeka na tutarudi kwa kishindo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalize tena kukushukuru kwa fursa hii na kwa kumpongeza sana na kumtia moyo ndugu yangu, Mheshimiwa Waziri Nape na timu yake. Sisi tunaokujua vizuri, waswahili wanasema haja ya mja kunena, muungwana ni vitendo. Si haki kuhukumiwa kwa neno moja kukosekana kwenye hotuba wakati kazi unaifanya ya kusukuma soka la nchi hii na sisi wote tunakujua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kuchangia katika hoja hii.
Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja na timu yao nzima, kwa kazi nzuri wanayoifanya na kwa hotuba nzuri waliyoitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba nafarijika sana kwamba kama Taifa, sasa tumefika tuna mjadala kuhusu matumizi ya rasilimali ya asili, ikiwemo ardhi kwa maendeleo yetu. Nafarijika kwamba sasa tuna mjadala kuhusu uhusiano kati ya mazingira na maendeleo, naamini kwamba mjadala huu unaweza kufanywa kwa busara, kwa hekima, bila jazba, wala vitisho ili tuweze kupata muafaka katika jambo hili muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, toka awali ni kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ya wakulima, Serikali ya wavuvi, Serikali ya wafugaji, Serikali ya watu wanaofanya shughuli zote katika nchi hii. Asiondoke mtu na dhana hapa, kwamba Serikali ya Awamu ya Tano au Waziri katika Serikali ya Awamu ya Tano anapendelea kundi moja au lingine katika Taifa letu. Hilo siyo kweli na halipo tumechaguliwa na watu wote, tumechaguliwa na kura za Watanzania wote.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1961, kwenye Mkutano uliofanyika Arusha mwezi Septemba, Rais wa Tanganyika wakati ule Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alitoa hotuba ambayo ndiyo iliweka msingi wa uhifadhi ambao tunaendelea nao leo, Mwalimu Nyerere alisema, inaitwa Arusha Manifesto, kipande kimoja kizuri sana ambacho kwa kifupi kilisema, kwamba sisi kama Taifa tumepewa dhamana ya kuhifadhi wanyama pamoja na maeneo ambayo wanyama wanaishi na tumepewa dhamana hiyo kwa ajili ya enjoyment ya hivyo vitu, lakini pia kwa sababu ya uhai na maisha yetu yanayokuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhifadhi wa misitu na uhifadhi wa wanyamapori, siyo kwa ajili ya misitu, siyo kwa ajili ya wanyamapori peke yake. Hifadhi ya misitu na hifadhi ya wanyamapori una uhusiano wa moja kwa moja na upatikanaji wa mvua na upatikanaji wa mvua, una uhusiano wa moja kwa moja na maendeleo ya kilimo, upatikanaji wa mvua una uhusiano na upatikanaji wa malisho. Kwa hiyo, hifadhi ya misitu ina uhusiano na ustawi wa ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, misitu inatoa huduma za kiikolojia ambazo zinafanya nchi yetu ipumue. Sasa hapa kumekuwa na mjadala, kana kwamba uhifadhi na ufugaji ni kama lila na fila hazifungamani. Uhifadhi na ufugaji siyo dichotomous, tunaweza kufanya vyote kwa wakati mmoja na tukafanya vizuri kabisa. Kuna dhana inajengwa kwamba hapa kuna ukinzani kati ya ufugaji na utalii. Msingi premise ya huo mjadala siyo sahihi. Kama Taifa tuna uwezo wa kufuga na kunufaika na ufugaji na tuna uwezo wa kuhifadhi na kunufaika na manufaa ya uhifadhi. Isijengwe dhana kwamba hizi ni shughuli zinazokinzana kwa hiyo lazima tuchague moja siyo kweli, kwa miaka yote tumekuwa tunafanya mambo yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilio sahihi cha wafugaji ni kwamba, kila mfugaji apatiwe eneo na amilikishwe eneo la kufuga, kilio sahihi cha wakulima ni kwamba kila mkulima apatiwe eneo na amilikishwe na hii ndiyo ahadi yetu Chama cha Mapinduzi, kwamba kila mfugaji na kila mkulima atamilikishwa eneo lake ili wafanye shughuli zao kwa tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo cha migogoro inayozungumzwa siyo shughuli watu wanazofanya. Chanzo cha migogoro inayozungumzwa ni kwamba maeneo haya hayakupimwa na ndiyo maana Waziri Mheshimiwa Lukuvi alikuja katika hotuba yake na mpango mkubwa wa matumizi ya ardhi pamoja na upimaji wa ardhi ambao utapelekea kupunguza migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha msingi sisi kama Taifa ni kwamba shughuli zile ambazo tunaamini zinaharibu mazingira ni lazima zifanyike kwa tija. Inawezekana kabisa kwamba kwenye kilimo, katika heka moja kama tutaweza kupata tani nyingi zaidi za mahindi, basi haihitajiki ardhi kubwa zaidi ili kuweza kupata manufaa. Vilevile katika ufugaji inawezekana kabisa kwamba ukafuga katika eneo na hautalazimika kutafuta eneo lingine lakini ukanufaika na manufaa ya ufugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili ufugaji udumu kwa miaka 100 ijayo, lazima tuhakikishe kwamba tunalinda kile tunaita natural capital. Katika dunia hii nchi zinatofautiana na utajiri wa rasilimali asili. Tanzania tunayo, inawezekana hatuna mtaji mkubwa wa kifedha, lakini tunao utajiri mkubwa wa natural capital, tunaweza tukaamua hapa Bungeni kwamba basi tufuge vizuri kwa miaka 20 ijayo, lakini baada ya hapo hakuna ufugaji tena, hakuna kilimo tena na hakuna mazingira tena. Kwa hiyo, katika mambo ambayo Serikali inayapanga kuyafanya, ni kuhakikisha kwamba shughuli hizi watu wetu wanazofanya zinadumu katika miaka mingi ijayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu mfumo wake wa kiikolojia una mito na mabonde mengi ambayo ndiyo yanafanya maisha yetu yawezekane, tunayo mito mikubwa Mto Pangani, Mto Ruvu, Mto Ruaha na mingineyo. Sehemu kubwa ya vyanzo vya mito hii ni kwenye maeneo yaliyohifadhiwa. Tukitaka Taifa letu life, mito hii itoweke, mabonde haya ambayo yana-sustain uhai wetu yatoweke, basi tusijali hifadhi ya misitu na hifadhi ya maeneo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja kwamba watu wameongezeka, mifugo imeongezeka, kwa hiyo basi tugawe. Ukweli ni kwamba kwa sababu hiyo kwamba watu wameongezeka ndiyo uhifadhi unahitajika zaidi. Katika nchi ndogo kisiwa Uingereza wamehifadhi asilimia 25 pamoja na kuwa na tatizo kubwa la ardhi katika ile nchi, asilimia 25 imehifadhiwa na bado maisha yanaendelea nasi kadri tunavyoendelea kama Taifa, shughuli zetu zitakuwa za tija zaidi na zitaondoka katika matumizi ya ardhi zaidi, na tutaweza ku-sustain maisha yetu bila shaka yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hapa bila shaka yoyote, kwamba binadamu ndio tunasemekana kwamba ni wanyama wenye akili kuliko wanyama wote. Tukishindwa kuhifadhi rasilimali asili, zinazowezesha maisha yetu leo, tukishindwa kuhifadhi rasilimali asili kwa watoto wetu na wajukuu wa wajukuu wetu, basi heshima yetu binadamu kama mnyama mwenye akili kuliko wote itabidi itiliwe shaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja kwa kusema kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inawajali wakulima na wafugaji katika usawa wao. Serikali ya Awamu ya Tano haipo hapa kusema shughuli hii ni bora kuliko shughuli ile nyingine, ili mradi shughuli inaendesha maisha ya watu wetu kwetu ni shughuli muhimu na tutahakikisha kwamba wanayoifanya wananufaika. Wakati huo tunahifadhi nchi yetu kwa sababu sisi tumekabidhiwa tunapita, kuna wajukuu wetu na wajukuu wa wajukuu zetu watakuja kupita, na watakuja kutushangaa, kwamba urithi tuliopewa sisi tulioachiwa na waliotuachia nchi hii, tumeuharibu kana kwamba ndiyo watu wa mwisho kuishi katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kubwa nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza. Napenda nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu - Balozi Mlima, watendaji wakuu, watumishi na maafisa wote wa Wizara ya Mambo ya Nje kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kazi yangu ya kwanza baada ya shule nilikuwa Afisa wa Mambo ya Nje, daraja la II, chumba changu kilikuwa 132. Katika Wizara hapa nchini kwetu au taasisi zenye kiwango cha juu cha uweledi wa utendaji ni pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje. Tunayo fahari kubwa ya kusema kwamba utamaduni huo wa uweledi na professionalism umeendelea na umezidi kuimarika chini ya Waziri mpya na Serikali mpya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vitu wanavyohitaji wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Nje kutoka katika Bunge hili ni support, ni kuungwa mkono kwa sababu wanatuwakilisha nje ya nchi wanabeba bendera yetu. Foreign policy (Sera ya Mambo ya Nje) ni extension ya domestic policy, ni extension ya mambo tunayotaka kuyafanya, ni kiwezeshi cha malengo ya maendeleo ya Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Serikali hii iingie madarakani sasa hazijafika siku 180. Kwa hiyo, hukumu iliyotolewa leo dhidi ya Serikali hii hasa kwenye hotuba ya Upinzani kwamba hatukufanya vizuri kwenye Sera ya Mambo ya Nje ni hukumu ambayo siyo ya haki kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mambo mengi yakiwemo masuala ya uteuzi wa Mabalozi. Kwanza nadhani Waziri pia atalieleza, procedure ya uteuzi wa Mabalozi inabidi uielewe kabla hujatoa hukumu ya aina ya Mabalozi wanaoteuliwa. Vilevile Rais Magufuli ameteua Mabalozi watatu tu tangu aingie madarakani. Amemteua Dkt. Asha Rose Migiro, Dkt. Dau na Chikawe na taratibu za uteuzi zinaeleweka na huwezi kuniambia katika hawa walioteuliwa hakuna mwenye sifa ya kushika nafasi ya Ubalozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba kuna baadhi ya mambo ambayo tunaruhusiwa kuyafanyia siasa lakini suala la hadhi na heshima ya watu Rais anaowatuma kutuwakilisha nje ya nchi siyo ya kufanyia siasa. Hawa watu tunapowatuma kule nje wanabeba bendera yetu sisi, Bunge hili halipaswi kutumika kuwadhalilisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi mkuu wa Sera ya Mambo ya Nje ni kulinda, kutetea na kusukuma maslahi ya Taifa katika mawanda ya kimataifa. Unapoihukumu Serikali hii katika mambo ya Sera ya Nje lazima useme ni wapi, ni lini na ni kwenye jambo gani tumeshindwa kutetea maslahi ya nchi yetu. Huwezi kuihukumu Serikali hii kwenye Sera ya Mambo ya Nje ukashindwa kusema ni kwenye jambo gani, ni lini na ni wapi tumeshindwa kulinda na kutetea maslahi ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yangu ni kwamba wenzetu hawakusema hayo mambo kwa sababu hakuna, tumeweza na tumefanikiwa. Kwa sababu ingekuwepo mahali ambao tume-fail tungeona kwenye hotuba yao. Tangu Serikali hii iingie madarakani katika mikutano yote na katika forum zote ambazo maslahi ya Tanzania yalihusika tuliwakilishwa na tuliwakilishwa kwa mafanikio makubwa iwe ni Paris, New York na kwingine kokote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Mambo ya Nje haiendeshwi kwenye vacuum bali inaendeshwa katika context ya sifa ya nchi, katika context ya sifa ya Rais na katika historia ya nchi. Sifa ya Tanzania duniani ni nzuri na sifa ya Rais wetu duniani ni nzuri na sifa ya Tanzania leo ni nzuri zaidi kutokana na kazi nzuri anayoifanya Rais hapa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Rais ameamua kuweka mambo sawa hapa ndani, kazi nzuri anayoifanya ndani inazidi kufungua fursa na milango kwa nchi yetu nje na kwa Watanzania waishio nje. Moja ya nyenzo kubwa ya diplomasia ni reputation na sifa ya kiongozi. Sifa ya Rais wetu imeiongezea sifa nchi yetu, imewezesha kazi ya nje ya nchi ambayo wenzetu hawakuifanya vizuri. Kwa hiyo, unaposema Rais hasafiri wakati huo huo kazi anayoifanya inawezesha Sera yetu ya Mambo ya Nje iende vizuri kunakuwa hakuna mantiki hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba moja ya matunda ya kazi nzuri ya Wizara ya Mambo ya Nje ni kwamba sasa hivi sisi tuko kwenye viwanda, ndiyo msingi mkuu wa mpango wetu wa maendeleo ya miaka mitano. Nchi ya China imechagua nchi nne Afrika ambapo itahamishia sehemu ya viwanda vyake. Nchi hizo ni Ethiopia, Kenya, South Africa na Tanzania. Hilo halikutokea kwa ajali, halikutokea kwa kurusha karata, limetokea kutokana na jitihada nzuri za wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Nje na limetokana na kazi nzuri anayoifanya Rais wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya urithi tunaoachiwa na viongozi waliotutangulia ni sifa ya nchi. Moja ya wajibu wetu viongozi wa siasa bila kujali vyama ni kuulinda urithi. Tunao wajibu Wapinzani na sisi kwenye Serikali na Chama Tawala kulinda urithi tulioachiwa na waliotangulia kwenye nchi hii.
Unapoitukana nchi yako ndani ya Bunge unajitukana wewe nje kwa watu tunaowawakilisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mchezo mmoja wa Shakespeare unaitwa Macbeth na nataka nizungumze kwenye quote moja kwenye act five inasema:-
“Life is but a walking shadow, a poor player,
That struts and frets his hour upon the stage,
And then is heard no more.
It is a tale told by an idiot, full of sound and fury,
Signifying nothing”. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni is full of sound and fury amounting to nothing. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa kuzungumzia suala alilolizungumzia Mheshimiwa Jaku na Mheshimiwa Keissy Mohamed. Nchi yetu sisi ni ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar. Baadhi ya kauli tunazozitoa humu ndani lazima ziheshimu Muungano wetu. Mheshimiwa Keissy Mohamed ni Mbunge wa CCM lakini lugha aliyoitumia sisi kama Serikali hatuikubali na Mheshimiwa Jaku vilevile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inafanya mambo makubwa matatu katika concern walizoleta. Kwanza, Ofisi ya Rais, Utumishi imetoa Waraka wa kuwezesha taasisi za Muungano zitengeneze utaratibu wa mgawanyo wa watumishi wa umma kutokana na quota iliyokubalika ya asilimia 79 na 21. Nimewaandikia Mawaziri wenye taasisi za Muungano kuhakikisha kwamba tunatimiza agizo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Tume ya Pamoja ya Fedha ilitengeneza mapendekezo kuhusu mgawanyo wa mapato na vyanzo vya mapato ya kuchangia shughuli za Muungano. Tumetengeneza Waraka wa Baraza la Mawaziri kwa ajili ya mgawanyo mpya kupitiwa ili tuweze kupata mgawanyo unaoakisi ukubwa wa uchumi na idadi ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, sasa hivi Zanzibar kwa makubaliano inaweza kutafuta misaada yake yenyewe nje ya Tanzania. Hayo ni mafanikio makubwa yaliyotokana na Serikali yetu katika kuimarisha Muungano wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yake na naunga mkono hoja hii.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuchangia. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara; kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kuandaa bajeti hii. Nawapongeza sana Wabunge wa CCM kwa kutimiza wajibu wao waliotumwa na wananchi wao kwa kutimiza sababu yao ya kuchaguliwa kwa kuingia Bungeni kufanya kazi waliyotumwa na wananchi na kueleza shida za wananchi wao mbele ya Serikali, nawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo kadhaa ambayo ningependa kuyazungumzia, la kwanza ni suala la VAT kwa Zanzibar na Bara. Kuna upotoshaji mkubwa sana kwamba hatua iliyochukuliwa na Serikali, hatua nzuri kabisa ya kuhakikisha kwamba bidhaa zinazozalishwa Tanzania Bara kwenda Zanzibar VAT inakusanywa Zanzibar; na bidhaa zinazozalishwa Zanzibar na kuletwa Tanzania Bara VAT inakusanywa Tanzania Bara. Kuna upotoshwaji mkubwa sana unaofanywa na wenzetu kule Zanzibar kwamba hatua hiyo inaiumiza Zanzibar, si kweli, ni kunyume chake. Hatua hii inainufaisha Zanzibar, hatua hii itawaumiza wale wadanganyifu wachache, waliokuwa wanatumia utaratibu huu kujipatia kipato ambacho sio halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ambalo ningependa kulizungumzia ni ahadi ya Chama cha Mapinduzi kwenye Ilani yetu kwamba kila kijiji kitapatiwa shilingi milioni 50 kwa ajili ya uwezeshaji, ukopeshaji wa wajasiliamali. Ahadi hii ya CCM ni hatua kubwa ya kimapinduzi ya kumuondoa Mtanzania katika lindi la umaskini. Mzunguko wa shilingi milioni 50 katika kijiji ni pesa nyingi sana zitakazoleta chachu ya maendeleo pale kijijini. Serikali katika mwaka huu wa fedha kama ambavyo mmeona, imetenga shilingi bilioni 59 kama kianzio, lakini zaidi ya hapo Serikali imeunda jopo la wataalam ambalo linatengeneza utaratibu madhubuti kabisa. Utaratibu utakaozingatia uzoefu wetu huko nyuma wa mifuko mbalimbali na mafanikio ya mifuko hiyo ili tuwe na utaratibu mzuri utakaohakikisha fedha hizi zinatumika kama zilivyopangwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni jambo kubwa linabidi lifanyike kwa umakini na umahiri mkubwa ili tusipoteze fursa hii adhimu katika kuwaokoa watu wetu. kwa hiyo utaratibu mzuri unaotengenezwa na Serikali utaletwa hapa Bungeni ili kabla ya kutumika na ninyi Waheshimiwa Wabunge muwe na mchango wenu katika aina ya utaratibu ambao Serikali itautumia na ikiwezekana kabisa aidha ni kwa kuleta Sheria mpya au kufanya mabadiliko ya Sheria katika Sheria ya Uwezeshaji sasa hivi. Ili fedha hizi ziwe katika msingi wa kisheria na ziweze kutumika vizuri kuliko mifuko mingine yote huko nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli kwamba zimetengwa shilingi bilioni 59, haina maana kwamba tutashindwa ndani ya miaka mitano kufanya vijiji vyote; tumeweka hizi ili tuanze na tujifunze na kadri tutakavyokuwa na utaratibu mzuri, kasi ya kupanga fedha nyingi zaidi ili tutimize ahadi hii kwa miaka mitano inakuwepo. Kwa hiyo napenda kuwahakikishiwa Waheshimiwa Wabunge na watanzania, kwamba hii ni ahadi ya CCM, hii ni ahadi ya Rais na itatimia bila shaka yoyote.
Naomba niseme kidogo jambo moja muhimu. Sisi Chama cha Mapinduzi tulipomteua Dkt. John Pombe Magufuli kuwa mgombea wetu, tulitoa statement duniani kwamba tunahitaji aina mpya ya nchi kutokana na aina ya kiongozi huyo. Kwetu sisi kumteua yeye tulitoa kauli duniani kwamba tunataka mabadiliko ya kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko ya kweli hayawezi kuletwa kwa hatua ndogo ndogo, mabadiliko ya kweli yanaletwa hatua kubwa na yanaletwa na uthubutu na uthubutu huo umeanza kujidhihirisha katika bajeti ya mwaka huu, tumethubutu kwamba tunaweza kukusanya shilingi trilioni 29.5; tumethubutu kwamba tunaweza kutenga asilimia 40 kati ya hizo kwa maendeleo. Unapothubutu jambo kubwa kuna watu watatia shaka, sisi wana CCM Serikali hii ni ya kwetu, Bunge hili ndio wengi, ilani ni ya kwetu, tusitetereke katika uthubutu wetu wa kukusanya shilingi bilioni 59 tumsaidie Rais tuisaidie nchi yetu kufikia malengo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa suala la hatua za kikodi hapo mbalimbali imetokea malalamiko kwamba kodi ni kubwa, kodi ni nyingi zitadhohofisha uwekezaji. Jambo hilo si la kweli kwa sababu utafiti unaonyesha mimi hapa ninayo ripoti inaitwa Tax incentive in a global perspective inasema kwamba; survey analysis shows that host country taxation and international investment incentives generally play only a limited role in determining the international pattern of FDI. Factors like market characteristics, relative production costs and resource availability explain most of the cross-country variation in FDI inflows. Transparency, simplicity, stability and certainty in the application of the tax law and in tax administration are often ranked by investors ahead of special tax incentives.
Suala siyo kiwango cha kodi, suala ni mfumo wa kodi. Kwa hiyo, miaka yote tumeaminishwa kwamba ukiweka kodi ndogo wanakuja, ukiweka kodi kubwa hawaji, dhana hiyo si ya kweli. Ukitengeneza mambo mengine vizuri zaidi ndiyo wanakuja ikiwemo uhakika wa mfumo wa kodi. Kwa hiyo, tusiwatishe wananchi na tusitishane hapa kwamba kiwango cha kodi tulichoweka kitafukuza wawekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ngoja nimalize kwa kusema kwamba Rais Magufuli tumempa usukani wa kuiongoza nchi yetu, lakini nchi hii ni yetu sote na sisi tunawajibu wa kumsaidia ili tufanikiwe. Rais Magufuli akifanikiwa, nchi yetu imefanikiwa sisi tusiwe kama watazamaji kwamba ngoja tumuone atafanyaje, sisi tuko naye kwenye basi hili tumsaidie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua tunazochukua nchi yetu ni sawasawa na gari nzuri aina ya benzi iliyoingia kwenye matope tunataka kuirudisha kwenye lami, hatua ya kuirudisha kwenye lami itakuwa na misukosuko, kuna wengine wataamua kushuka lakini tuendelee kuwa ndani ya gari hilo mpaka likae kwenye lami lifike safari. Maendeleo yanahitaji sacrifice, katika bajeti hii Wabunge sisi tume-sacrifice, tume-sacrifice kwa kukubali kukatwa kodi, kila mtu lazima a-sacrifice, wafanyabiashara, waendesha bodaboda, kila mmoja lazima a-sacrifice ili nchi yetu iende mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema mwaka 1961 wakati Rais Kennedy wa Marekani anaapishwa aliwaambia wa Marekani kwamba ask not what your country can do for you, but what you can do for your country. Ni wakati sasa kwa Watanzania wote kutokaa siku zote na kujiuliza nchi hii itanifanyia nini bali sisi tutaifanyia nini nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kutoa mchango. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Hawa Ghasia pamoja na Kamati yake kwa kazi nzuri waliyoifanya naunga mkono hoja waliyoitoa na mapendekezo waliyoyapendekeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wote tunafahamu kwamba Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliongoza nchi yetu hii kwa miaka 24 na tangu ametutoka ni miaka 17 na siku zote bado amebaki kuwa rejea ya masuala mbalimbali ya uongozi wa Taifa letu na kwa kweli amekuwa kama sehemu ya uongozi wa nchi kwa maana ya reference hata akiwa kaburini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini imekuwa hivyo? Je, ni kwa sababu ameifikisha nchi yetu kule kwenye ndoto kabisa ya maendeleo makubwa ya kiuchumi, hapana. Ni kwa sababu dhamira yake ya kutufikisha huko ilikuwa wazi na ilieleweka pamoja na kwamba hatukufika kule tulikokuwa tunatarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais Dkt. Magufuli sasa hivi ana miezi 15 tu ya uongozi wake. Dhamira ya kutupeleka kwenye nchi ya neema hamna mtu yeyote anayeweza kubisha katika Bunge hili kwamba ipo. Dhamira iko wazi, ni nzuri na inaeleweka.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu sasa hivi na Serikali ya Awamu ya Tano ina miezi 15 tu madarakani kati ya miezi 120 ambayo tunatarajia Rais aiongoze nchi yetu. Leo tunachojadili ni robo tu ya bajeti ya kwanza kamili ya Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo, hamna ubishi kabisa kwamba kuna improvement kwenye kila eneo la utendaji wa Serikali na unapojenga misingi, unapoimarisha misingi ili mbele iwe rahisi kabisa kutengeneza mambo yawe rahisi nafahamu kuna watu watapata shaka watakuwa na uwoga, watapinga. Naamini kwamba nchi hii ni yetu sote na wakati mwingine unasikitika kwamba inapotolewa habari mbaya hapa Bungeni au habari ya kusikitisha, kwa mfano tunaposema Benki fulani imepata hasara nashangaa kuna watu wanapiga makofi kana kwamba hiyo ni habari ya kufurahisha. Nchi hii ni nchi yetu sote, habari ya kusikitisha ni yetu sote. Wawe Wapinzani, wawe watu wa CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tusifike mahali tukaamini kwamba mambo yanapotokea na kunapotokea setbacks basi kuna watu wanapaswa kufurahia. Nchi hii ni yetu sote, watu tunaowaongoza ni wetu sote, hivyo, naamini kabisa kwamba mtu yeyote mwenye akili timamu hawezi akasimama leo akasema nchi yetu imerudi nyuma badala ya kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ndugu amesimama amezungumza kuhusu Zanzibar kwamba kuwe na mazungumzo, tukae, kaka yangu Mheshimiwa Mtulia. Sasa uchaguzi Zanzibar ulikwishafanyika, Serikali ilishapatikana, Serikali halali, imechaguliwa kwa kura halali na ni muhimu kutambua kwamba Serikali ile ni ya Umoja wa Kitaifa kwa sababu kuna vyama vinne ndani ya Serikali ile na Serikali ile iko tayari kuzungumza…
MWENYEKITI: Malizia, malizia.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilinde muda wangu umeliwa.
Wenzetu watusaidie kwamba tuzungumze na nani kwa sababu CUF ziko mbili, tuzungumze na ipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuzungumze na ile iliyochukua ruzuku au ile nyingine?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi uliyonipatia ya kuchangia hoja zilizowasilishwa leo. Nianze kwa kuwapongeza sana Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwanza kwa taarifa yao nzuri kwenye eneo letu lakini pia kwa kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya katika kipindi chote ambapo tumekuwa tunafanya nao kazi. Tunawapongeza na kuwashukuru sana wametupa ushauri, miongozo na tumeelekezana na tumefanya kazi nzuri. Kwa hiyo, Mwenyekiti aliyetangulia na Mheshimiwa Murad sasa na Wajumbe wote hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa mambo mengi kwenye taarifa lakini nitazungumza mawili tu kutokana na uchache wa muda. Kwanza, ni suala zima la uwezo wa kifedha na fedha zinazotolewa kwa ajili ya usimamizi wa mazingira nchini. Nadhani wote tunakubali kwamba jambo hili tumelizungumza katika vikao mara nyingi kuhusu umuhimu wa hifadhi wa mazingira lakini uwezo mdogo wa rasilimali wa kufanya zile kazi zinazotakiwa kufanywa na Kamati ya Bunge imelieleza hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ambacho naweza kuliambia Bunge lako Tukufu ni kwamba tunaendelea kuzungumza ndani ya Serikali kati yetu sisi, Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Fedha kuhusu namna ya kudumu ya kuweza kupata fedha za hifadhi ya mazingira kwa vyanzo mahsusi. Tulianza mwaka juzi kwa kupendekeza maeneo kadhaa ya mapato ambapo kufanyika kwa hizo shughuli moja kwa moja kunaathiri mazingira. Kwa mfano, mapato yanayotokana na magogo, mkaa na uingizaji wa bidhaa ambazo zinachafua mazingira, basi asilimia kadhaa ya mapato hayo iende kwenye Mfuko wa Mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo hayo yamewasilishwa kwenye Kamati ya Think Tank ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha, yametafakariwa na baadhi yametafakariwa na Kamati ya Bajeti ya Bunge katika Bunge lililopita. Imani yetu ni kwamba ndani ya Serikali tutamaliza mazungumzo ili mwaka ujao wa fedha sasa pale tutakapokuwa tumeelewana basi tutakuja na mapendekezo ya vyanzo vya kudumu na vya uhakika kwa ajili ya Mfuko wa Mazingira ili tuweze kuwa uwezo na nguvu kubwa ya kusimamia Sheria ya Mazingira lakini kurekebisha pale maeneo ambapo mazingira yatakuwa yameharibika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi dhamira yetu ni pale Wabunge katika Majimbo yao watakapokuwa wanaona changamoto ya mazingira, basi iwe rahisi kwao wanapotuambia sisi, sisi tuweze kujibu kwa uharaka tukiwa na uwezo wa fedha wa kusaidia kurekebisha mazingira yanayoharibika. Kwa hiyo, hii ni kazi yetu sote sisi ndani ya Serikali lakini pia Wabunge kama watu wenye sauti na wenye uwezo wa kupanga fedha tushirikiane ili tuweze kuhakikisha kwamba Mfuko huu unajaa fedha ili tuweze kufanya mambo ambayo Wabunge wanataka tuyafanye na mambo mengine ambayo tunaendelea kuyafanya ikiwemo kutafuta fedha kutoka kwenye vyanzo mbalimbali huko duniani na kwa washirika wetu wa maendeleo wa Kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la mifuko ya plastiki, limezungumzwa hapa na limezunguzwa kitambo humu Bungeni na Kamati yetu ya Bunge imelitafakari na tumetafakari kwa pamoja sisi pamoja na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara. Nataka kusema kwamba katika taarifa ya Kamati ya Bunge mtaona imeeleza kwamba nchi yetu viwanda vyote vilivyopo nchini mwaka jana 2016 vilizalisha tani 73.6 za mifuko ya plastiki lakini pia taarifa hiyo hiyo inasema mifuko ya plastiki iliyoingizwa kutoka nje ni tani 1,354. Kwa hiyo, utaona kwamba asilimia zaidi ya 90 ya mifuko ya plastiki inatumika nchini ni ile iliyotoka nje ya nchi siyo inayozalishwa ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna utata wa takwimu kuhusu idadi ya watu ambao wameajiriwa katika viwanda hivi kwa sababu kama viwanda viko 46 vinazalisha tani 73 kwa mwaka maana yake kila kiwanda kinazalisha chini ya tani moja na nusu kwa mwaka jambo ambalo kidogo ni gumu kulitafakari. Kwa hiyo, sisi kama Serikali tutaendelea kulishughulikia jambo hili na Kamati ya Bunge imeelekeza kwamba tupige marufuku uingizaji wa mifuko kutoka nje ya nchi ili hatimaye tuelekee katika kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba jambo hili lina implications kikodi, kiajira na kadhalika lakini sisi kama Serikali au sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais tumeona kwamba madhara ya matumizi ya mifuko ya plastiki ni makubwa katika mazingira na afya ya watu wetu. Kwa hivyo basi, tutashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Fedha, bahati nzuri Sheria ya Mazingira, kifungu cha 80 kinampa mamlaka Waziri mwenye dhamana ya mazingira kwa kushirikiana na kushauriana na Waziri mwenye mamlaka ya fedha kutengeneza nyenzo za kiuchumi zitakazoweza kushamirisha mbadala wa bidhaa zinazoharibu mazingira. Kwa hiyo, nitazungumza na mwenzangu wa Wizara ya Fedha tuone nyenzo zipi za kiuchumi zitakazotusaidia ili tutakapopiga marufuku mifuko ya plastiki basi kuwe na uchumi mpya wa mifuko mbadala na huko ndiko tunakoelekea na ndiko huko tunakotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu jirani zetu karibu wote wamepiga marufuku mifuko ya plastiki lakini hawajapiga marufuku uzalishaji wa mifuko ya plastiki. Kwa hiyo, mifuko ya plastiki kwa mfano kwenye nchi moja ya jirani hawaitumii pale lakini wanaizalisha na hawajafunga viwanda kwa sababu sisi tunaruhusu. Kwa hiyo, sisi tumekuwa ni dampo la mifuko ya plastiki. Tunaamini kwamba tutakapozuia na sisi matumizi ya mifuko ya plastiki basi hata mianya inayotumika kuingiza mifuko hii nchini mwetu na yenyewe itazibwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni uamuzi mkubwa ambao utaathiri maisha ya watu na namna wanavyoishi lakini naomba tu niseme kwamba tukubali na tuwe tayari kuupokea uamuzi huu wakati wowote. Wale wenzetu wenye viwanda tulishatoa tahadhari tangu mwezi Mei mwaka jana kwamba uamuzi huu unakaribia na tutakapofika tu kwamba kufanya uamuzi huu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja nimalizie.

Wenzetu wanaozalisha na kuingiza mifuko ya plastiki itakapofika wakati Serikali itakapofanya uamuzi wa kupiga marufuku isije ikasemekana kwamba hatukuwa na taarifa ya kutosha. Hapa Bungeni katika Kiti hiki hiki mwezi Mei mwaka juzi 2016, tulitoa taarifa kuhusu dhamira hii ya Serikali. Kwa hiyo, tunaomba tu wajiandae kwamba tutafikia huko

lakini kama nilivyosema Serikali yetu kwa kujua kwamba lazima kupatikane mbadala basi itatengeneza mazingira ya kushamirisha uzalishaji wa mifuko mbadala ili watu wetu wasipate shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, naunga mkono mapendekezo ya Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, taarifa ya Kamati. Nianze kwa kuipongeza Kamati kwa kazi nzuri ambayo imeifanya na kwa taarifa nzuri ambayo imeitoa. Pia nishukuru Mwenyekiti wa Kamati na Wajumbe kwa ushirikiano mzuri ambao wamekuwa wanatuonesha, kwa msaada ushauri na maelekezo mbalimbali, ambayo wamekuwa wanatupatia, kwa hiyo nampongeza sana Mwenyekiti, Mheshimiwa Sadiq Murad pamoja na Kamati yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali tunayapokea Maazimio yote ya Kamati yanayohusu mazingira kama yalivyoandikwa kwenye ripoti ya Kamati, ambayo yapo ukurasa wa 81 na 82 ambayo yanahusu mazingira. Ni maazimio mazuri na hatuna mabadiliko yoyote katika hayo maazimio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nizungumzie mambo mawili matatu tu yaliyojitokeza kwenye taarifa ya Kamati ambayo labda yanahitaji maelezo kidogo. La kwanza lipo kwenye ukurasa wa 57 ambapo Kamati imesema, kuwa kutegemea gesi ya LPG kama nishati mbadala ni kuwaumiza Watanzania kwa kuwa bei ya nishati hii ni kubwa na inaendelea kupanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka hili jambo likae sahihi kwenye kumbukumbu za Bunge na Wabunge kwa ujumla, kwamba ukiangalia takwimu za matumizi ya nishati hapa nchini, nishati ya LPG ni moja ya nishati ambazo bei yake inashuka kila mwaka. Mtungi wa kilo tano, kilo sita mwaka uliopita ulikuwa Sh.21,000, sasa hivi ni Sh.17,000. Mtungi wa lita 15 ulikuwa Sh.55,000, sasa hivi Sh.45,000 na tunaona trend kwamba uwekezaji na usambazaji kwenye LPG unaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya sekta ambazo hazithaminiwi kwa ukuaji mkubwa lakini zinakuwa kwa kasi ni hii ya nishati ya LPG. Kwa hiyo, nataka tu ieleweke wazi kama sisi kama Serikali tunaunga mkono wawekezaji katika tasnia hii na tunaamini kwamba sisi na wenzetu wa Wizara ya Nishati ambao wanahusika na udhibiti tutachukua hatua za kisera kuhakikisha kwamba tunailea tasnia hii ili ikue na Watanzania wapate nishati hii ya LPG ya gesi ya mitungi kwa bei nafuu na mahali popote walipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani jambo la msingi kujua kwamba, nchi yetu bado kwa sehemu kubwa inategemea rasilimali asili kwa maendeleo yake, kwa shughuli za kilimo, shughuli za ufugaji na nyinginezo. Kwa hiyo, uhifadhi wa mazingira katika haya maeneo una nafasi kubwa zaidi ya kuisaidia nchi yetu. Napenda Bunge lichukue uongozi kama ambavyo Kamati imechukua uongozi katika kuhakikisha kwamba masuala ya mazingira yanatiliwa maanani sana katika mipango yetu ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunaongea hapa na Naibu Waziri wangu, tunahesabu Wabunge waliochangia hii Kamati ni wangapi wamegusa masuala ya mazingira, ni Wabunge watatu tu. Tunajua kwa sababu ya umuhimu wa masuala ya viwanda na biashara, lakini nataka niseme bila hifadhi ya mazingira hakuna viwanda na biashara. Tunataka tuseme kwamba Tanzania, Waheshimiwa Wabunge, naomba tusikilizane tafadhali! Tanzania ni moja ya nchi tano zinazoongoza duniani kwa kukata misitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku inayoenda kwa Mungu kila dakika, kila siku, tunakata misitu kwa kiwango cha kiwanja cha mpira, kila dakika, kila siku; kila dakika inayopita hapa Tanzania, misitu inayofyekwa ni size ya kiwanja cha mpira wa miguu. Hizi takwimu zimeanza kuchukuliwa mwaka 2010. Kwa hiyo, fikiria kwa miaka tisa mfululizo kila dakika unakata size ya kiwanja cha mpira wa miguu, asilimia 61 ya nchi yetu inakaribia kuwa jangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kwa uchumi ya land degradation, forest degradation ni takriban shilingi bilioni 2.2 dollar kwa mwaka kwenye uchumi au asilimia ya GDP. Kwa hiyo, hatua hizi zote tunazochukua za kuisukuma mbele nchi yetu kimaendeleo, kama hatutahifadhi mazingira zitakuwa ni za bure, kabisa. Kama hatutachukua hatua madhubuti za kuhifadhi mazingira, kilimo, uvuvi, ufugaji itakuwa ni bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku hizi kuna mbinu mpya ya kupima utajiri wa nchi na utajiri wa watu, inaitwa natural per capita natural resource capital, yaani maliasili hizi za nchi nzima zinathaminiwa na kila Mtanzania anapewa kwa per capita, thamani yake. Kwa miaka 20 iliyopita utajiri wa maliasili wa kila Mtanzania umeshuka kwa asilimia 35. Kwa hiyo hizi physical asset zinaongezeka, lakini natural capital, utajiri wa maliasili wa kila Mtanzania unapungua kwa asilimia 35 katika kipindi cha miaka 20 iliyopita. Kwa hiyo, kwa sababu idadi yetu inazidi kuongezeka kwa kasi, hili jambo ni la muhimu na la kulitazama. Kwa hiyo, ningependa Bunge lako lichukue uongozi kwenye eneo hili la hifadhi ya mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo limezungumzwa hapa ni lile suala la mita 60 na athari zake kwa shughuli za watu na maelekezo ya Mheshimiwa Rais yaliyotoka ya kutazama sheria hizo ili kuweza kuruhusu watu wafanye kazi. Ni dhahiri kabisa kwamba Watanzania wengi wanategemea maeneo chepechepe, mbogamboga nyingi tunazokula mijini michicha, cabbage na nini vinazalishwa kwenye maeneo haya na maeneo haya pia yanatoa; ukienda kule kwa ndugu zangu, kule kwetu kwa Bwana Shangazi tunaita vitivo, ukienda kule kwa ndugu zangu kwa akina Mwamakamba kule unyalukolo wanaita vinyungu na kadhalika. Kwa hiyo tunaelewa kwamba kuna baadhi ya Watanzania wanategemea haya maeneo ya chepechepe kwa ajili ya maisha yao na Serikali za Mitaa zinapata kodi humo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kutokana na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, tayari Wizara sita tutakaa na kuangalia namna gani tunaweza kuhakikisha kwamba ruhusa inatolewa huku hifadhi ya mazingira ikizingatiwa. Moja ya nyenzo tulizonazo ni Kifungu cha 57 cha Sheria ya Mazingira, kinasema kwamba:

“Kwa kuzingatia Kifungu cha (2) ndani ya mita sitini hakutafanyika shughuli yoyote ya binadamu ya kudumu au ambayo kwa asili yake inaweza kuharibu mazingira…”

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sheria imepiga marufuku shughuli ndani ya mita sitini. Kifungu hicho hicho cha 57(2) kinasema: Waziri, kwa maana ya Waziri mwenye dhamana ya mazingira, anaweza kuweka miongozo ya kuendesha shughuli za binadamu ndani ya maeneo hayo yaliyoelekezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua hilo nililolisema awali, sheria yenyewe imeweka uwezekano wa Serikali kuruhusu shughuli kufanyika kwa masharti maalum. Kwa hiyo, sisi kama Ofisi ya Makamu wa Rais na kwa mamlaka niliyopewa kama Waziri mwenye dhamana ya Mazingira, tutaweka miongozo ya kuendesha shughuli za kibinadamu katika haya maeneo; miongozi ambayo itazingatia hifadhi ya mazingira, lakini pia upatikanaji wa riziki za watu. Kwa hiyo tutaweka namna ambayo kwa mfano aina ya mazao unayoweza kulima, ukaribu na kwenye kingo, matumizi ya mbolea za kemikali, ruhusa ya kutoingiza udongo kwenye mto na kadhalika. Miongozo hii itakuwa technical na itatumika kuzuia jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili jambo linawezekana kufanyika, hakuna contradiction hapo kwa sababu sheria yenyewe imetoa ruhusa hiyo na tutaitumia sheria hii kuhakikisha kwamba azma ya Kiongozi wetu inatimia, lakini azma vilevile ya hifadhi ya mazingira inatimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa nafasi uliyonipa ya kutoa mchango na mimi katika hoja iliyoko mezani, namshukuru Mungu kwa neema zake na baraka zake za afya na uhai na leo tumeuanza mwezi Mtukufu wa Ramadhani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa naongea mara ya kwanza tangu uchaguzi uishe, napenda kuwashukuru wananchi wa Bumbuli kwa heshima waliyonipa ya kuendelea kuwa Mbunge wao. Nampongeza pia Mheshimiwa Spika, wewe Naibu Spika, Wabunge wote waliochaguliwa na wananchi kwa kuaminiwa na dhamana hii kubwa na muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza wetu mpya Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan kwa kushika hatamu za uongozi wa nchi yetu. Nampongeza ndugu yangu Dkt. Philip Mpango kwa kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais, nawapongeza Mawaziri wote kwa imani ambayo Marais mawili wameonyesha kwao na tunawatakia heri na baraka wakifanikiwa katika kazi zao nchi yetu na sisi imefanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo mawili napenda kuyazungumza leo siku ya leo. La kwanza ni mambo ya Jimboni kwangu Bumbuli; mambo ya barabara, umeme, kiwanda chetu cha chai na kadhalika na la pili ni suala zima la umoja, mshikamano, utulivu na upendo miongoni mwetu na nitaanza na hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe pole za dhati kabisa kwa sababu tunaelekea mwisho wa arobaini kwa Watanzania kwa kuondokewa na kiongozi wetu jasiri na shupavu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Pole zaidi kwa familia hasa mama Janeth na Watoto. Msiba huu umetuingiza katika kipindi cha mpito ambacho hatukukitarajia na mpito siku zote una mashaka, wasiwasi, hofu, mshtuko na huzuni. Kwa hiyo wananchi kote waliko wana hayo mambo ya hofu, shaka, mshtuko, huzuni na wasiwasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi ambacho Watanzania wanahitaji uongozi wetu, sisi ambao ni viongozi, ni sasa. Bahati nzuri Mheshimiwa Rais wetu mpya ametoa kwa kauli zake na vitendo vyake, ametoa mwelekeo mpya ambao unaleta matumaini mapya ya kutupunguzia huzuni, mashaka, mshtuko na wasiwasi. Mwelekeo alioutoa Mheshimiwa Rais una sehemu nne: Ya kwanza ni kupunguza maumivu ya jeraha la msiba; sehemu ya pili ni kutuunganisha Watanzania; sehemu ya tatu ni kuendeleza mema na mazuri aliyofanya Rais wetu aliyepita; na sehemu ya nne ni mwelekeo alioutoa Mheshimiwa Rais ni kufanya maboresho, marekebisho na mabadiliko pale panapostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama leo kwa heshima na tahadhima mbele ya ninyi viongozi wangu kutoa wito wangu kwamba nasi tujielekeze huko katika mwelekeo huo huo ambao ameutoa Mheshimiwa Rais. Kipindi ambacho nchi yetu inahitaji umoja, utulivu na mshikamano ni sasa. Kkauli za utengano, kauli za kutiliana shaka, kauli za kutuhumiana, kauli za kuhukumiana, hazijengi na zinawachanga wananchi. Mambo makubwa aliyoyafanya Rais wetu aliyepita Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli hayatafutika, hayatafutwa, hayatapotea na hayatapotezwa kwa kauli yeyote ya kubezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale miongoni mwetu ambao wanatoa maoni na ushauri wenye nia njema wa kuweka mambo sawa, wa kuyatengeneza vizuri, wasibezwe, wasihukumiwe katika dhamira zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhamira ya kauli na ushauri na maoni ipo ndani ya moyo wa mtu. Mtu anaposifu kwamba mama Samia ameanza vizuri asihukumiwe kwamba anatafuta cheo, anapokosoa isionekane ni nongwa na anapokaa kimya isionekane amesusa. Naomba sana tusihukumiane katika dhamira za kauli na vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi aliyotufanyia Rais Dkt. Magufuli naweza kuichukulia kama vile ametushonea nguo nzuri kabisa ya kupendeza, akitokea mtu akaona kwamba ile nguo kuna uzi umejitokeza tuukate, isionekane dhambi; akijitokeza mtu akasema katika hii nguo kifungo kimelegea hebu tukiweke vizuri, isionekane huyo mtu ni msaliti. Mtu huyo anapofanya kazi hiyo ya kukaza kifungo au kukata uzi, nguo ikapendeza, bado sifa ni ya mshonaji. Kwa hiyo, naomba sana kwa sababu dalili nilizoziona sio nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kwamba sisi kama viongozi tunayo haki na wajibu wa kutoa maoni kuhusu mambo yetu yaendeje, lakini njama, vikundi, vigenge vya kuweka mashinikizo kwamba kipi kifanyike, hatua zipi zichukuliwe, zipi zisichukuliwe, si sawa kabisa na haitujengei umoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uongozi wa nchi ni jukumu kubwa na la kihistoria, Rais wa nchi yetu ana madaraka na nguvu na mamlaka makubwa sana na kwa vyovyote vile katika uongozi wake anaacha alama. Mwalimu Nyerere ameacha alama, Mzee Mwinyi ameacha alama, Mzee Mkapa ameacha alama, Kikwete ameacha alama na Rais Dkt. Magufuli ameacha alama, ndio asili ya urais. Sasa wajibu wetu sisi kama viongozi tuliopo ni kulinda yale mema ambayo viongozi wetu wameyafanya kuanzia wakati wa Mwalimu, mpaka Rais Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tupiganie kuyalinda yaliyofanywa na Rais Magufuli, lakini tusipigane wakati tunafanya hivyo. Tukipigana kwa mambo ya nyuma, tutashindwa kupigania mambo mazuri ya mbele ambayo Rais mpya anataka kuyafanya. Vikumbo vya nani ni mnazi zaidi wa Rais Dkt. Magufuli, nani mnazi zaidi wa Rais Samia na viwiko vikali ambavyo watu wanataka kupigana havisaidii wala kujenga. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele ya pili imegonga.

MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba upendeleo wa dakika tatu nimalizie.

NAIBU SPIKA: Hapana, majina ninayo mengi sana hapa mbele, ahsante sana.

MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na makubwa mbele…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba tuheshimiane, tusihukumiane na tumsaidie kiongozi wetu, tuwe na umoja na upendo kwa sababu utulivu ndani ya Bunge ndio utasaidia kiongozi wetu atawale vizuri. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa fursa hii. Nami nitumie nafasi hii kuipongeza Wizara kwa kazi nzuri inayofanya. Sisi kwetu katika Jimbo la Bumbuli tuna changamoto za vijiji vingi ambavyo havina umeme, lakini nimeongea na viongozi wa REA na Wizara na wametoa ahadi kwamba maeneo yote ambayo hayana umeme yatafikiwa.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya leo kwenye Wizara hii ni suala la nishati ya kupikia. Nishati ya msingi kuliko zote ni nishati ya kupikia. Kila nyumba kunapikwa na kila siku kunapikwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mahitaji ya nishati hapa nchini unaweza usiwe na umeme wa kupigia pasi au wa kuwasha taa au wa kupooza vinywaji lakini lazima utafute nishati ya kupikia. Kwa hiyo, tunapozungumza suala la nishati kama wawakilishi wa wananchi hatuwezi hata siku moja kuacha kuweka mkazo na msisitizo wa nishati ya kupikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa Tanzania asilimia 92 ya Watanzania wanatumia nishati inaitwa tungomotaka (biomass), yaani kuni na mkaa kupikia. Naomba nirudie; asilimia 92 ya Watanzania wanatumia kuni na mkaa kupikia. Ukichukua matumizi yote ya nishati katika shughuli zote hapa nchini iwe mafuta, gesi, hydro bado nishati ya tungomotaka (biomass) kwa maana ya kuni, mkaa, pumba na kadhalika ni asilimia 80, inashinda hata mafuta yote kwenye magari na mitambo na inashinda hydro zote. Naomba nirudie; ukichukua total primary energy consumption hapa nchini, energy zote tulizoweka kama mitambo na kadhalika bado energy ya tungomotaka ndiyo inaongoza. Ushauri wangu kwa Wizara, nafahamu iko Sera ya Nishati, lakini kutokana na ukubwa na umuhimu wa biomass (tungomotaka) yaani kuni na mkaa, lazima kuwe na sera tofauti ya kutusaidia kama Taifa kuendesha eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, thamani ya mnyororo wa biashara ya mkaa hapa nchini ni kubwa kuliko thamani ya export za mazao yetu yote; ni kubwa kuliko kahawa, chai au korosho. Thamani ya mnyororo wa mkaa, value chain ni karibu dola bilioni moja, siyo biashara ndogo. Revenue ya mkaa Dar es Salaam peke yake mwaka jana ilikuwa ni karibu shilingi bilioni 800; hii ni sekta kubwa mno ambayo kama Serikali na kama Wizara hatuwezi kuipuuza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafahamu kuna hoja kwamba tunasambaza umeme vijijini ili tunusuru misitu ili umeme utumike kupika. Mji unaoongoza kwa usambazaji wa umeme hapa nchini ni Jiji la Dar es Salaam, asilimia karibu 96 ya Jiji la Dar es Salaam lina umeme. Hata hivyo, mji unaoongoza kwa matumizi ya mkaa hapa nchini ni Dar es Salaam ambapo asilimia 70 ya mkaa wote unaotumika Tanzania unatumika jiji moja. Kwa hiyo, kwa hoja hiyo, itachukua muda mrefu sana kwamba huu umeme tunaousambaza ndiyo utuokoe kutoka kwenye matumizi ya mkaa na kuni. Kwa hiyo, zinahitajika jitihada za makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inasemekana mkaa ni nishati ya wanyonge. Ni kweli lakini si kweli; humu Wabunge wengi na viongozi na watu wenye uwezo mzuri wa fedha wananunua mkaa, lakini wananunua kwa gunia, wanyonge wananunua kwa kopo. Kwa hiyo, ukipiga hesabu, chakula ambacho nimetumia mimi kwa mkaa wa 70,000, mnyonge anakuwa ametumia kwa 180,000 kwa sababu ananunua kwa kopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa suala la kuni na mkaa na nishati ya kupikia limekaa maeneo mengi. Biashara ya mkaa inadhibitiwa na TFS (Wakala wa Misitu Tanzania) ambao ipo Wizara ya Maliasili na Utalii; Sera ya Nishati ya Nishati ambayo inahusika na mambo ya nishati ya kupikia iko Wizara ya Nishati; masuala ya hifadhi na mazingira yapo Ofisi ya Makamu wa Rais. Kwa hiyo, naamini kwamba huu mkanganyiko na mtapakao wa udhibiti wa jambo hili muhimu ukifanyiwa kazi vizuri, basi tunaweza kupata manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kama viongozi wa wananchi katika jambo ambalo tunaweza kuwatendea haki Watanzania ni kuhakikisha kwamba tunaondoa umaskini wa nishati, unaitwa energy poverty.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JANUARY Y. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa fursa hii uliyonipa. Nami niungane na wenzangu kuwashukuru sana Wabunge wote waliochangia hoja hii na waliochangia kwenye eneo linalohusu sekta ya nishati.

Mheshimiwa Spika, yaliyochangiwa ni mengi, muda uliopo wa kuyajibu yote hautoshi. Kwa hiyo, tutayajibu kwa maandishi namba moja, namba mbili tutayajibu wakati wa bajeti yetu ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi tu niseme kwa baadhi ya mambo hasa ndugu zetu wa Mikoa ya Iringa na Njombe kwenye masuala ya nguzo nataka niwahakikishie kwamba nitaenda wiki inayokuja tutakaa, tutayamaliza, tutaelewana kabisa bila wasiwasi wowote na mazao yao yatanufaika na ununuzi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye mambo mawili hasa bei ya mafuta. Kwenye sekta ya mafuta kwa ujumla kuna masuala mawili, kuna bei na upatikanaji. Suala la bei limeongelewa kwa kirefu sana ikiwemo na Mawaziri mbalimbali, sababu na mwenendo wa bei ya mafuta umeongelewa.

Mheshimiwa Spika, mwenendo wa bei ya mafuta katika miezi 16 iliyopita umekuwa ni wa kupanda na umepanda katika nchi zinazozalisha mafuta na nchi zinazoagiza mafuta vilevile. Nchi ya kwanza katika uzalishaji wa mafuta duniani ni Marekani na kwenyewe hata huko bei imepanda. Kwa hiyo, mwenendo ni wa kupanda tofauti ni kwa kiwango na kasi, lakini tofauti pia ni je, hatua zinachukuliwa?

Mheshimiwa S[ika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha juzi aliongelea kuhusu hatua za kikodi kwenye jambo hilo. Mimi nitaongelea hatua za muda wa kati na mrefu katika kuhakikisha kwamba tunahimili katika kipindi kirefu na cha kati bei kubwa ya mafuta.

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu tumekuwa na ndoto ya kuwa na hifadhi ya kitaifa ya kimkakati ya mafuta. Hatimae mwaka huu ndoto hiyo itatimia, tunaandika kanuni za kuiwezesha kuwepo vilevile tumepata washirika katika uwekezaji wa miundombinu ya ushushaji na uhifadhi wa mafuta ili kuwezesha hifadhi hiyo kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, ndani ya Serikali tunazungumza kuhusu kuanzisha Mfuko wa Kuhimii Ukali wa Bei za Mafuta ambao ni Fuel Price Stabilization Fund ambayo katika siku zijazo itatusaidia kutuokea katika nyakati kama hizi.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunaendelea na mazungumzo na wauzaji na wazalishaji mafuta hasa nchi rafiki ambao tuliyaanza tangu mwezi Oktoba mwaka jana ili tuone katika kipindi hiki kama tunaweza kupata nafuu ya kununua mafuta huko moja kwa moja. Kwa hiyo, kuhusu masuala mengine nje ya kikodi Wizara yetu inayafanyia kazi karibu kila siku.

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa suala la mfumo wa ununuzi wa mafuta kwa pamoja hapa mchango umetolewa, bulk procurement system, bahati nzuri mfumo huu ulikuja kutokana na mapendekezo na maelekezo ya Bunge mwaka 2011 na mimi nilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini wakati huo na Bunge kwa kauli moja likaishauri Serikali kuanzisha mfumo huo. Mfumo huo ukaanza na umekuwepo kwa kipindi cha miaka 10. Sasa mfumo huu umewekwa na watu, unaendeshwa na watu. Tumepokea ushauri mzuri sana wa Waheshimiwa Wabunge kuhusu kuuboresha mfumo huu. Nasi tupo tayari tumepokea ushauri huo na kama kuna taarifa zozote zinazohusu udhaifu katika mfumo huo na namna ya kuchukua hatua pale kwenye mapungufu basi tuko tayari wakati wote kupokea na kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu siyo Msahafu siyo Quran siyo Biblia unaweza kubadilishwa wakati wowote ili kutusaidia pale ambapo tunadhani utakuwa na manufaa makubwa kwa nchi. Kikubwa tu ni kuwa na mfumo ambao utatuhakikishia uhakika wa kupatikana kwa mafuta lakini na bei ambayo inahimilika.

Mheshimiwa Spika, wapo Waheshimiwa Wabunge wamesema kwamba wanao uwezo wa kuisaidia nchi kupata mafuta ya bei nafuu, kwamba yako baharini huko na meli, sisi tunasema mtu yeyote, pahala popote, Mtanzania yyyote mwenye taarifa au uwezo wa kuisaidia nchi kuleta mafuta ya bei nafuu karibu sana ofisini hata leo ili tuzungumze hilo jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kung’ang’ania kitu kumbe kuna kitu kingine kitatusaidia Zaidi, nchi hii hi yetu wote hatuna shaka yoyote. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge njoo ofisini, kikubwa tu ni kwamba hizo meli zilizopo zituhakikishie kwamba mafuta hayo yataingia consistence kwa wakati wote kuhakikisha kwamba supply ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ni upatikana wa mafuta. Ni muhimu…

SPIKA: Sekunde 30.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Spika, katika janga kubwa linaloweza kutokea ni kukosekana mafuta. Bei ni jambo tunaweza tukalizungumza lakini kukosekana mafuta kwenye vituo, kuwepo na foleni, kuwepo na vigaloni kwenye majumba yetu ni hatari kubwa zaidi. Nataka niwahakikishie Watanzania kwamba kwa nchi yetu ukilinganisha na majirani zetu mafuta yakutosha yapo juu ya kiwango cha kanuni tulizoweka ya siku 15. Kwa hiyo, mafuta yapo na Serikali itahakikisha kwamba yanaendelea kuwepo ili uchumi usisimame. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami naunga mkono hoja. Nakushukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia katika Taarifa hizi za Kamati hasa katika Taarifa ya Kamati ya Nishati na Madini. Nianze kwa kuwapongeza Kamati kuanzia Mwenyekiti, Mheshimiwa Kitandula, Makamu Mwenyekiti, Mheshimiwa Gulamali na Wajumbe wote kwa kweli kwa kazi nzuri na taarifa nzuri waliyoitoa, lakini vile vile kwa siku zote kuwa makini katika kushauriana na sisi na kusaidiana katika kupeleka mambo mbele yanayohusu sekta yetu na taarifa yao kama alivyosema Mheshimiwa Dotto Biteko, inadhihirisha umahiri, umakini na weledi iliyonayo Kamati katika kushughulikia mambo ambayo wanashughulika nayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nami ni mchangiaji siyo mjibuji wa hoja na napenda
nitambue mchango mzuri sana wa Mheshimiwa Manyinyi, Mheshimiwa Nusrat, Mheshimiwa Tabasam, Mheshimiwa Iddi Kasim, Mheshimiwa Genzabuke na Mheshimiwa Issaay na niseme yale ambayo wameyaelekeza kwetu kama Wizara, basi tutayachukua na kuyafanyia kazi. Kwa kuwa muda hautoshi kuyazungumzia yote lakini niseme tu nimeyapokea, nimeyaandika na tutayashughulikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda haraka haraka tu kuhusu REA nafahamu ni kweli kuna malalamiko mengi na changamoto nyingi kuhusu ucheleweshaji wa Miradi ya REA. Naomba nitoe faraja kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote wa Tanzania kwamba baada ya kubaini changamoto zilizopo tumebadilisha utaratibu sasa wa manunuzi, usimamiaji, ufuatiliaji na tathmini ya miradi hii. Kuanzia sasa kwa mfano, vigezo vya mkandarasi kupata mradi vitakuwa tofauti kwamba mkandarasi hawezi kupata mradi mpaka alionao walau amefikia 60%.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutakuwa na pre- qualification kama Kamati ilivyopendekeza kwamba kutakuwa na kundi la wakandarasi mahiri ambao watakuwa wamepitia vigezo na kazi zitakuwepo, atakayemaliza haraka ndiyo atapata kazi nyingine haraka. Hii itatoa incentive kwa wakandarasi kufanya kazi haraka. Sasa hivi haijalishi kama una kasi au huna kasi, unaingia kwenye tenda, unapata kazi nyingine. Kwa hiyo matokeo yake ni kwamba wakandarasi wamejilimbikizia kazi kwenye eneo letu la REA lakini kwa sababu ni wakandarasi wako kwenye madaraja na kwingineko, kwa hiyo unakuta wana kazi nyingi kuliko uwezo wa kuzifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia taarifa nyingine kwa Kamati ni kwamba rasmi sasa REA tumeajiri vijana 136 ambao kazi yao itakuwa ni usimamizi wa Miradi ya REA tu katika majimbo ya Waheshimiwa Wabunge. Hawa watakuwa hawana kazi nyingine zaidi ya kufuatilia na kuripoti kwa Wabunge na Serikalini kuhusu mwenendo wa utekelezaji wa miradi hii. Hawa watakuwa ni kiungo muhimu kati yetu sisi Wizarani, REA, TANESCO na viongozi wa kisiasa ili wakati wote tuwe katika ukurasa mmoja kuhusu changamoto zilizopo na tuweze kusaidiana kuzimaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kwenye Miradi ya Ujazilizi; hata tutakapomaliza kupeleka umeme kugusa vijiji vyote, bado kutakuwa na vitongoji vingi vitakuwa havina umeme. Kwa mfano, kwenye vijiji sasa hivi tuko 80% lakini kwenye vitongoji tuko 44%. Kwa hiyo utaona jinsi gani kufikia vijiji tafsiri yake siyo kupeleka umeme kwa watu wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi kama Serikali tumeamua kuja na mpango mkubwa wa kupeleka umeme katika vitongoji vyote ambao tutaufanya ndani ya miaka mitano. Ilikuwa tuanze mwaka wa fedha uliopita 2021/2022, tulipata changamoto kwa sababu ni fedha nyingi. Tutakuja wakati wa bajeti kuwaomba mtusaidie Waheshimiwa Wabunge kupitisha mpango huo kabambe na ambao utatekelezwa kwa namna tofauti kama inavyotekelezwa miradi ya sasa, kwani kwa sasa hivi ina changamoto. Kwa hiyo, mradi huu sasa utajibu maswali mengi ya ujazilizi kwa sababu utafikisha umeme katika maeneo yetu mengine yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie shilingi 27,000 na shilingi 300,000, niseme tu taarifa imekuja kwetu na kwa sababu ya muda, tunaishughulikia na tutatoa mwongozo maalum wa namna ya kulifanya jambo hili. Jambo ambalo nilitaka Waheshimiwa Wabunge walifahamu, ni kwamba, gharama halisi ya kumwingizia mtu umeme kwenye nyumba yake ni shilingi 426,000 mpaka shilingi 800,000. Kwa hiyo, shilingi 27,000 ni chini sana ya gharama halisi. Shilingi 331,000 bado iko chini sana ya gharama halisi. Kwa hiyo, Serikali inatoa subsidy kwa kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, unapotoa shilingi 27,000 maana yake Serikali kupitia TANESCO inatoa ile ya ziada. Hii pesa inatoka katika shughuli nyingine za maendeleo ambazo tulikuwa tuzifanye. Kwa hiyo, ni muhimu tunapotaka hizi bei tujue gharama yake, na sisi tutakuja na mpango.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu umeme kukatika, niseme tu kwamba tunafahamu na tunakiri changamoto bado ipo. Ambacho nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania ni kwamba hivi tunavyoongea tunayo mipango madhubuti ya kuifumua grid nzima na kuirekebisha. Kwa sababu changamoto kubwa iliyokuwepo ni miundombinu chakavu. Hili jambo ukubali ukatae, ndiyo ukweli kwamba miundombinu yetu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme ilikuwa haitoshelezi mahitaji na haijafanyiwa marekebisho muda mrefu. Tarehe 15 Februari tutasaini mradi unaitwa Gridi Imara, ni miradi 26 ya takribani shilingi trilioni moja ku-stabilize grid yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, tutawaalika mshiriki kwa sababu ni jambo ambalo litaenda kuanza safari ya kumaliza changamoto ya miundombinu, na uzalishaji wa umeme tunaongeza ili tusiwe na gap.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Julius Nyerere unaenda vizuri, tunashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao wamefika na wameona na wametushauri kuhusu namna ya kwenda vizuri. Ni kweli kulikuwa na changamoto ya transmission line, miundombinu ya kutoa umeme kule kuusambaza kuingiza kwenye grid. Mradi huu ulianza kutekelezwa Desemba 2018, lakini tulisaini njia za kutoa umeme pale Septemba, 2021 miaka mitatu, kulikuwa na gap. Ila tumeharakisha mpaka sasa kufikia asilimia 80, siyo jambo dogo. Kwa hiyo, mradi wa uzalishaji umeme utaisha pamoja na mradi wa kutoa umeme kwenye eneo lile na kuusambaza kwenye gridi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo ya mafuta ya Mheshimiwa Tabasam tumeyapokea. Kama mnavyofahamu, hivi juzi juzi Serikali ilisaini mkataba wa uwekezaji mkubwa wa miundombinu ya kupakua na kuhifadhi mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Sekunde 30 malizia.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane kukubali mapendekezo ya Kamati na kuyaunga mkono na kuendelea kuahidi ushirikiano wa Wizara, Bunge na Kamati ya Bunge kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari za Mwaka 2016
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kuchangia hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuanze na kitu gani ambacho hakipo kwenye mjadala. Jambo ambalo halipo kwenye mjadala leo ni umuhimu wa vyombo vya habari na umuhimu wa waandishi wa habari. Kwa sababu nimeona naona jana tumetumia muda mrefu sana kuzungumza kuhusu umuhimu wa vyombo vya habari na umuhimu wa waandishi wa habari, sote tunakubaliana katika hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wameenda mbali kwa kulinganisha waandishi wa habari sawa na taaluma nyingine, Madaktari, Wahandisi, nami nakubaliana na hilo, kwamba kwa hapa tulipofikia kwa umuhimu wa taaluma ya uandishi wa habari, kwa umuhimu wa tasnia ya habari katika ujenzi wa demokrasia, umuhimu wake ni sawa na taaluma zile nyingine ambazo tunazitaja kwamba, ni muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukishakubaliana hivyo kwamba, uandishi wa habari ni taaluma muhimu kwa vyovyote lazima tukubaliane kwamba, lazima kuwe na udhibiti wa Serikali katika taaluma hii na tasnia hii muhimu kwa sababu, huwezi kusema kwamba, uandishi wa habari ni muhimu sana sawa na uhandisi lakini ukaishia hapohapo. Kwa maana hiyo basi, tasnia hii, taaluma hii iendeshwe shaghalabaghala bila udhibiti mahususi, bila kuwepo na mamlaka na sheria inayoweka viwango. Kwa hiyo, sheria hii imeenda kutekeleza hisia zetu, kwetu sisi, tasnia ya habari ni muhimu kwa nchi yetu, ndiyo maana tumeweka udhibiti, tumeweka viwango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda turudi kwenye dhana ya udhibiti kwa ujumla. Hapa kihistoria katika nchi yetu kuna baadhi ya huduma na biashara ambazo zimekuwa zinadhibitiwa na msingi wa udhibiti huo ni maslahi mapana ya jamii kutokana na shughuli zile. Kwa mfano, tunadhibiti huduma ya mawasiliano, tunadhibiti dawa, tunadhibiti shughuli nyingine muhimu; sasa msingi wa udhibiti wa tasnia hii ni kwamba, ipo njia panda kati ya huduma kwa demokrasia kwa upande mmoja, lakini vilevile biashara kwa upande mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uandishi wa habari na tasnia ya habari inatoa huduma kwa demokrasia ya nchi yetu, lakini wakati huohuo ni biashara vilevile. Kwa hiyo, hii dhana ya kuachia self regulation wakati kuna hatari kubwa kwamba, ile self regulation inaweza ikatumika vibaya na maslahi ya kibiashara yakachukua nafasi kubwa zaidi katika udhibiti kuliko huduma kwa demokrasia. Ndiyo maana tumeamua kwamba, Serikali angalau kwa sasa ndiyo ambayo ipewe nafasi ya kuweka viwango, kwa hiyo hii ni muhimu kufahamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi ambazo zimeendelea katika tasnia ya habari zilishajaribiwa namna zote, kule Marekani, Uingereza kwa mfano, kulikuwa na kitu kinaitwa Press Complaints Commission ambayo ilikuwa ni chombo cha self regulation katika tasnia ya vyombo vya habari, tasnia ya magazeti, lakini tunafahamu miaka karibu 16 iliyopita kile kitu kilivunjwa. Kilivunjwa kwa sababu, kilishindwa kuweka balance sahihi kati ya maslahi ya kibiashara ya wenye vyombo vya habari na maslahi mapana ya umma na kikaanzishwa chombo kingine mahususi kabisa madhubuti ambacho kiko chini ya Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti,vile vile katika nchi ya Norway ambayo wote tunaisifia kwamba ni nchi ambayo imeendelea kidemokrasia, inajali haki za binadamu, kwenye Wizara ya utamaduni na mambo ya kanisa (Ministry of Culture and Church Affairs) kuna kitu kinaitwa (Norwegians Media Authority), chombo cha Serikali, ambacho kinatoa leseni, kinadhibiti ubora, kinasema nani anunue chombo kipi na kwa kiasi gani; yote ni kwa ajili ya kuhakikisha kwamba jambo hili linaendeshwa kwa namna nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahi kwamba Mheshimiwa Lissu, hapa ametoa historia kwamba wakati wa chama kimoja, wakati vyombo vyote vya habari vinamilikiwa na Serikali, wakati hakuna magazeti mengine ya binafsi kulikuwa tayari na accreditation ya waandishi wa habari. Sasa anachotuambia ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, anachotuambia ni kwamba; ithibati haina uhusiano na kuminya demokrasia au kuminya sauti. Kama wakati wa chama kimoja ambapo hakukuwa na ushindani wala upinzani bado Serikali iliamua kuwe na viwango katika tasnia hii, dhana ni ile ile, kwamba kinachotakiwa hapa ni kuwa na viwango sahihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, unaposema kwamba sasa hivi Serikali inalileta jambo hili kwa sababu inataka iminye waandishi, au iminye tasnia ya uandishi inaenda kinyume na historia ambayo ameitoa mwenyewe kwamba hata huko nyuma jambo hili lilikuwa linafanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ningekuwa mwandishi wa habari, katika kutazama sheria hii ningejiuliza mambo mawili. Kwanza liability yangu katika shughuli yangu iko wapi, pili, je, sheria iliyowekwa inaruhusu au hairuhusu kwa kiasi gani watu kuivamia tasnia hii na kuiondoa thamani? Sasa uzuri wa sheria hii ni kwamba inatenganisha liability kwa kila kundi. Mwandishi liability yake iko peke yake na makosa ya mmiliki au mchapishaji hayawezi kuchukuliwa na mwandishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sheria nyingi za namna hii, huu ni ubunifu mkubwa kwenye sheria yetu kwa sababu unamlinda mahsusi mwandishi wa habari asiingie kwenye liability, asiingie kwenye matatizo kwa sababu ya makosa ya mtu mwingine. Ingekuwa mimi hili jambo lingekuwa la kusherekea na kufurahia na la kupongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, nadhani wenzetu, rafiki zetu ambao tunafanya nao kazi sisi kama Serikali, kama Chama Tawala, waandishi wa habari, ningependa na kufurahia utaratibu ambao unakinga hii taaluma isivamiwe na watu ambao wanaiondolea sifa. Sheria hii ndicho chombo kinachoweza kwa sababu sifa na heshima ya uandishi wa habari inaondolewa na watu wachache sana ambao hakuna sheria wala taratibu za kuwazuia wasiingilie. Kwa hiyo, ningekuwa mimi, ningefurahia exclusivity katika hii shughuli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia, best practices za jambo hili duniani kote, mwaka juzi Kenya walipitisha sheria wakaweka na dhamana kabisa (bond), kwamba ukitaka kuanzisha chombo cha habari unaweka fedha nyingi chini, ili pale utakapokutwa na makosa ikitoka judgment ile fedha inachukuliwa. Hapa sisi hatukuamua kufanya hivyo kwa sababu tuliona kwamba ni vyema watu wote wanaotaka kuingia kwenye biashara hii wapate fursa ya kuingia kwenye biashara hii bila kuwa na vikwazo, bila kuwa na upinzani wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani na naamini kwamba umefika wakati sasa kwenye baadhi ya mambo tukubaliane kama Taifa, kwamba lazima shughuli hii ambayo inaathiri sana maisha ya watu, uendeshaji wa demokrasia yetu lazima iendeshwe kwa utaratibu murua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma yalifanyika makosa ambapo haki za watu na nimshukuru ndugu yangu Mheshimiwa Zitto amesema yeye amekuwa mhanga mkubwa sana wa kuandikwa na kutukanwa na yeye anadhani ni sawa na ni sahihi, lakini kwa watu wengine ambao si wanasiasa, ambao hawako kwenye shughuli yetu sisi ambao tumezoea kusemwa na kutukanwa, uvumilivu wetu na nafasi yetu ya kuvumilia matusi tusiihamishie kwa watu wengine ambao hawana hatia wala hawana makosa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kumalizia nampongeza sana Waziri, kwamba ametengeneza historia kwa kutuletea sheria nzuri. Naamini kabisa tasnia hii ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Sisi tunapenda na tunategemea waandishi wa habari na uandishi wa habari kwa maendeleo na demokrasia ya nchi yetu, hakuna namna ambayo Serikali hii inaweza kuminya uhuru wa habari. Kama kuna kitu ambacho Serikali hii inataka ni kupata msaada wa waandishi wa habari katika kupambana na rushwa na ufisadi na maovu yote katika jamii kwa sababu wao wana nafasi kubwa ya kuweza kuisaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii itawezesha waandishi wa habari waisaidie Serikali, wamsaidie Mheshimiwa Raisi wetu na chama chetu katika kuijenga jamii yetu upya na kujenga jamii nzuri. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, hongera sana na naamini kwamba tutaipitisha sheria hii na huko mbele kama kutakuwa na marekebisho tutayafanya yanapostahili, lakini kwa sasa kwa ilivyoandikwa ni nzuri na inastahili kupitishwa .
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.