Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Margaret Simwanza Sitta (40 total)

MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Urambo imebahatika kuwa na Mto Ugalla unaopita Kusini kwake kuelekea Mto Malagarasi ukiwa na maji ya kutosha.

Je, kwa nini Serikali isianzishe mradi wa kuvuta maji ya Mto Ugalla kupeleka Mji wa Urambo ambao unakuwa kwa haraka na wananchi wake wamekuwa wakikabiliwa na uhaba mkubwa wa maji kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mji wa Urambo unakuwa kwa haraka na wananchi wake wanakabiliwa na uhaba wa maji kwa muda mrefu. Katika kutatua tatizo la maji kwa Mji wa Urambo, Serikali imepanga kuupatia Mji huu maji kutoka chanzo cha Mto Ugalla.

Katika kutekeleza azma hii ya kutoa maji kutoka Mto Ugalla, Serikali imeendelea na upembuzi yakinifu ili kutathimini wingi wa maji na pia ili kupata muafaka na Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira kuhusiana na kutekeleza Mradi ndani ya Hifadhi ya Ugalla.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali imepanga kuanzisha mradi mwingine wa kutoa maji Mto Malagarasi kwa ajili ya kuleta maji Miji ya Urambo, Kaliua, Mji mdogo wa Nguruka, baadhi ya vijiji vilivyopo Wilayani Uvinza na maeneo mengine ya Wilaya ya Uyui, Manispaa ya Tabora na vijiji vitakavyokuwa umbali wa kilomita 12 kando kando ya bomba kuu. Mradi huu utasaidia kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wengi zaidi kwa kuwa Mto Malagarasi una maji mengi yanayotiririka wakati wote wa mwaka.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Mhandisi Mshauri anaendelea na kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina, pamoja na uandaaji wa makabrasha ya zabuni. Kazi hii ilianza mwezi Julai, 2015 na inategemewa kukamilika mwezi Februari, 2016. Aidha, katika mwaka huu wa fedha 2015/2016, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kazi ya usanifu wa mradi mkubwa na utekelezaji wa mradi mkubwa na utekelezaji wa miradi ya muda mfupi ya kuboresha huduma ya maji katika Miji ya Urambo na Kaliua.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Ujenzi wa Barabara ya Tabora – Ndono – Urambo ulikuwa unaendelea vizuri kabla ya shughuli hizo za ujenzi kusimamishwa ghafla kilomita tano nje ya mji wa Urambo kwa karibu mwaka sasa.
Je, ni lini ahadi ya Serikali ya kujenga kilomita nane kupitia katikati ya mji wa Urambo itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara ya Tabora – Urambo kwa kiwango cha lami umegawanyika katika sehemu mbili. Kuna Tabora - Ndomo ambayo ni kilometa 42 na Ndomo - Urambo kilometa 52. Ujenzi wa sehemu ya Tabora – Ndomo ulikamilika Februari, 2014 na barabara kukabidhiwa rasmi Februari 2015. Ujenzi wa sehemu ya Ndomo - Urambo unaendelea.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa sehemu ya Ndomo - Urambo unaendelea na utekelezaji umefikia asilimia 88.7 ambapo kilometa 46 zimekamilika kwa kiwango cha lami na mradi unategemewa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016.

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya barabara inayopita katikati ya mji wa Urambo, kilometa 6.3 haikuwa katika mkataba wa ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Ndomo – Urambo. Sehemu hiyo itajengwa kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Tabora katika mwaka wa fedha wa 2016/2017. Usanifu wa barabara na makisio ya gharama za ujenzi wa sehemu hiyo umefanyika. Hivyo baada ya kupata fedha, ujenzi wa kiwango cha lami wa sehemu hiyo utaanza.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Mfumo wa sasa wa kuwahudumia wakulima wa zao la tumbaku wa Wilaya ya Urambo na Mkoa wa Tabora kwa ujumla una mapungufu mengi yanayowaletea wakulima usumbufu kama vile bei za pembejeo kuwa kubwa kutokana na kuagizwa nje na riba kubwa za benki, masoko ya tumbaku kutokuwa na uhakika na hatimaye kusababisha kushuka thamani ya tumbaku, bei inayobadilika pamoja na uchache wa wanunuzi:-
(a) Je, ni kwa nini hasara inayotokana na matatizo hayo ibebwe na mkulima peke yake?
(b) Je, Serikali imejipanga vipi kuondoa matatizo hayo ili mkulima wa tumbaku anufaike na kilimo na hatimaye ajikwamue kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa yapo maeneo mbalimbali yanayomkosesha mkulima mapato. Maeneo haya ni pamoja na mfumo wa usambazaji pembejeo uliokuwa na mianya mingi inayosababisha madeni hewa, baadhi ya viongozi wa vyama kukopa fedha nyingi kupita uwezo wa vyama wa kuzalisha tumbaku na kadhalika. Kwa sasa Serikali imebadili mfumo huo na kuelekeza wagavi wa pembejeo hizo kuzifikisha moja kwa moja kwenye vyama vya msingi tofauti na utaratibu wa awali wa kupitisha pembejeo kwenye vyama vikuu. Aidha, ili kuwa na uhakika wa soko kilimo cha tumbaku nchini huendeshwa kwa mkataba kati ya wanunuzi na wakulima. Hivi sasa bei hupangwa kabla ya msimu wa kilimo kuanza ili mkulima ajue bei na kiasi anachotakiwa kuzalisha. Tatizo la soko na bei mara nyingi huwakumba wale wakulima wanaozalisha tumbaku bila kuwa na mikataba ambapo hujikuta tumbaku yao ikikosa soko au wakipewa bei ya chini.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kukabiliana na changamoto zinazomkabili mkulima wa tumbaku. Hatua hizo ni pamoja na kuboresha mfumo wa upangaji wa bei ya tumbaku ambapo wakulima upendekeza bei yenye tija kwao na kuiwasilisha kwa wanunuzi kupitia vikao vya Halmashauri ya Tumbaku yaani Tobacco Council. Bei hiyo hujadiliwa na hatimae kufikia muafaka. Mfumo huu wa upangaji wa bei umeanza kutumika rasmi msimu wa mwaka 2015/2016. Sanjari na maboresho ya mfumo huu Serikali inaendelea na jitihada za kuongeza wanunuzi wa tumbaku kutoka China ili kuongeza ushindani kumwezesha mkulima kupata bei nzuri. Aidha, Serikali itapitia tozo za pembejeo zinazoingia nchini na kuangalia uwezekano wa kuziondoa ili kumpunguzia mkulimba gharama ya uzalishaji.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. MARGARET S. SITTA) aliuliza:-
Je, ni sababu zipi zinazoifanya Serikali yetu iridhike na utaratibu wenye usumbufu mkubwa unaowataka wakazi wa Tanzania wanaotaka kwenda Uingereza watafute visa kupitia Kenya na Afrika Kusini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo awali huduma za viza zilikuwa zikitolewa na Ubalozi wa Uingereza, nchini. Ubalozi huo ulihamisha shughuli za utoaji wa viza kutoka hapa nchini kwenda nchini Kenya tarehe 1 Desemba, 2008 na kuanzia tarehe 18 Agosti, 2014 huduma hizo zimehamishiwa nchini Afrika Kusini na siyo Kenya tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Serikali ya Uingereza, uamuzi huo ni wa kisera na umefikiwa ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi wa Idara ya Viza na Masuala ya Uhamiaji ya Uingereza. Hivyo, mchakato wa utoaji visa za Uingereza unafanyika kikanda. Kwa mantiki hiyo, maombi yote ya viza kutoka
NAKALA YA MTANDAO (ONLINE DOCUMENT)
15
nchi zote za Afrika Mashariki na Kati, yanafanyiwa kazi katika Ubalozi wa Uingereza, nchini Afrika ya Kusini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, waombaji wa viza hapa nchini wanatakiwa kuwasilisha maombi yao na nyaraka zinazohitajika katika Kituo cha Kuombea Viza, (Visa Application Center) kilichopo Viva Tower Dar es Salaam. Kituo hicho ndicho chenye jukumu la kusafirisha maombi yao kwenda Afrika ya Kusini na kurejesha nyaraka husika kwa waombaji nchini. Mwombaji halazimiki kufuata huduma hiyo nchini Afrika ya Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Ubalozi wa Uingereza Nairobi unashughulikia maombi machache ya Visa (restricted number of applications) kwa viongozi wa Serikali na watendaji wengine wenye pass za Kidiplomasia hasa katika hali ya dharura. Maombi hayo yanapaswa kupelekwa moja kwa moja Ubalozi wa Uingereza Nairobi na waombaji wenyewe au kupitia Ubalozi wa Tanzania Nairobi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania wenzangu kwamba zoezi la utoaji visa lina utaratibu wake na moja ya taratibu hizo ni kwamba nchi inayotoa visa ina uhuru wa kuamua ni wapi itatolea visa hizo. Kwa mantiki hiyo, hata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupitia Balozi zake zilizopo nje, inazo taratibu zake za kutoa visa kwa wageni wanaotembelea Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema Watanzania ambao wangependa kutembelea nchi ya Uingereza wakazingatia taratibu zilizowekwa za nchi hiyo katika maombi ya visa ikiwemo kuomba visa mapema, kuwasilisha nyaraka zote muhimu na taarifa sahihi ili kuepuka usumbufu usio wa lazima.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Kushusha madaraka kwa wananchi (D by D) ni jambo muhimu sana katika masuala muhimu yakiwemo elimu, afya na kilimo na kadhalika.
Je, Serikali haioni kuwa ni mapema mno kushusha elimu ya kidato cha tano na sita kwenda TAMISEMI kabla ya kurekebisha changamoto za elimu za awali, msingi na sekondari hadi kidato cha nne?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ugatuaji wa madaraka (Decentralisation by Devolution) ni suala la Kikatiba kwa kuzingatia Ibara ya 145 na Ibara ya 146 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977 ambayo inatambua uwepo na madhumuni ya Serikali za Mitaa kuwa ni kupeleka madaraka kwa wananchi. Utekelezaji wake unafanyika kwa kuzingatia Sheria ya Serikali za Mitaa, Sura Namba 287 ambayo inazungumzia suala la Mamlaka za Wilaya na Sura Namba 288 - Mamlaka za Miji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kugatua elimu ya msingi na sekondari kwenda katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa ulikuwa ni kupeleka madaraka kwa wananchi ili kuwapa fursa ya kushiriki katika kusimamia na kuziendeleza shule hizo. Uendelezaji wa walimu kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita chini ya Mamlaka za Serikali za Mitaa umewezesha kubaini changamoto mbalimbali na kuzipatia ufumbuzi kwa haraka ikiwa ni pamoja na miundombinu na masuala ya kiutumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ifahamike pia kwamba uendeshwaji wa shule kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita hauwezi kutenganishwa kwa sababu sehemu kubwa ya shule hizo zina kidato cha kwanza hadi cha sita, lakini pia wananfunzi wanaofaulu kidato cha nne wanajiunga na kidato cha tano hapohapo shuleni au shule nyingine. Aidha, kwa kuzingatia matakwa ya Kikatiba na juhudi kubwa ya Serikali katika kuboresha elimu ni wazi kwamba suala la kidato cha tano na kidato cha sita kusimamiwa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ni muafaka sana. Kinachotakiwa ni kuunga mkono juhudi kubwa za Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli katika ukusanyaji wa kodi ili kujenga uwezo wa kutatua changamoto za kibajeti zilizopo.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Baadhi ya mambo ambayo yanamkosesha mkulima wa tumbaku mapato stahiki ni pamoja na tozo za pembejeo zinazoingizwa nchini na kuzifanya kuwa ghali, kuwepo wanunuzi wachache wa tumbaku na hivyo kudumaza ushindani wa bei na uwezo mdogo wa kifedha wa Bodi ya Tumbaku:-
(a) Je, Serikali imefikia hatua gani katika kuondoa utitiri wa tozo za pembejeo?
(b) Je, hadi sasa Serikali imevutia wanunuzi wangapi kutoka China na kwingineko?
(c) Je, kuanzia msimu wa 2016/2017 Serikali imeiongezea Bodi ya Tumbaku kiasi gani cha fedha katika bajeti yake ili iendeshe masoko ya tumbaku kwa ufanisi?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na bei kubwa ya pembejeo za kilimo, mifugo na uvuvi, Serikali imeunda Timu ya Kitaifa kupitia kodi na tozo mbalimbali katika pembejeo hizi ili kuona uwezekano wa kuzipunguza au kuziondoa kabisa. Kazi hii itakapokamilika, wananchi watafahamishwa.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Bodi ya Tumbaku bado inaendelea na mazungumzo na baadhi ya wanunuzi wa tumbaku kutoka China na Kampuni ya Sunshine kutoka China imeonesha nia ya kuwekeza katika ununuzi wa tumbaku nchini na imeshakamilisha taratibu zote hapa nchini. Kwa sasa kampuni hii inafuatilia kibali cha kuingiza tumbaku ya Tanzania nchini China. Katika hatua nyingine ya kuongeza ushindani katika soko la tumbaku, kampuni ya Japan Tobacco International imeanza ununuzi wa tumbaku msimu uliopita na imeongeza ushindani katika biashara ya tumbaku.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ufinyu wa bajeti, Bodi ya Tumbaku imekuwa ikipata fedha kidogo kutoka Serikalini ambazo hazikidhi mahitaji ya Bodi kuendesha shughuli zake ikiwa ni pamoja na zoezi muhimu la masoko. Kutokana na hali hiyo, msimu wa mwaka 2014/2015, wadau walichangia uendeshaji wa masoko ya tumbaku, lakini kwa sasa Bodi ya Tumbaku inatumia fedha zinazotokana na ada ya export permit inayolipwa na makampuni ya usafirishaji tumbaku nje ambayo ni asilimia 0.025 ya thamani ya tumbaku inayosafirishwa. Fedha hizi kwa sasa ndizo zinazosaidia Bodi kuendesha shughuli zake ikiwa ni pamoja na jukumu la kuendesha masoko.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Serikali ina mkakati wake wa kupata maji kutoka Mto Ugala ili kukabiliana na uhaba mkubwa wa maji katika Wilaya ya Urambo.
(a) Je, ni hatua gani zimechukuliwa hadi sasa katika kutekeleza ahadi hiyo na kiasi gani cha fedha kitatumika?
(b) Je, kiasi gani kimetengewa kwa mwaka mpya wa fedha?
(c) Je, ni lini mradi huu utafikisha maji Urambo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margatet Simwanza Sitta Mbunge wa Jimbo la Urambo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze wananchi wa Urambo kwamba wamechagua jembe. Mila za Kiafrika tunajua kwamba akina mama ndio wanaochota maji na huyu mama anahangaika sana na hadi leo asubuhi amekuja ofisini, hakunikuta. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutatua tatizo la maji kwa Mji wa Urambo Serikali ilipanga kupatia mji huu maji kutoka chanzo cha Mto Ugala. Katika hatua za awali za upembuzi yakinifu wa mradi, ulionekana Mto Ugala hukauka wakati wa kiangazi kati ya Juni na Oktoba. Kutokana na changamoto zilizotajwa, mpango wa Serikali wa kupeleka maji Urambo ni kutoka Mto Malagarasi na siyo Mto Ugala. Mradi huu unatarajiwa kugharimu kiasi cha dola za Marekeni 332.91.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga kiasi cha shilingi 500,000,000 kwa ajili ya kukamilisha usanifu wa mradi. Aidha, Serikali inaendelea kufanya mazungumzo na Shirika la Maendeleo la Ufaransa AfD kwa ajili ya kupata fedha za ujenzi wa mradi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi huo mkubwa utagawanywa katika lot nne ili kuharakisha utekelezaji wake. Kwa kufanya hivyo mradi unatarajiwa kufikisha maji Urambo katika kipindi cha Miaka miwili mara baada ya fedha kupatikana.
MHE. MUSSA R. NTIMIZI (K.n.y. MHE. MARGARET S. SITTA) aliuliza:-
Pamoja na jitihada za Serikali za kuendeleza kilimo, bado kuna vikwazo vinavyomkandamiza mkulima wa tumbaku ashindwe kujiendeleza kiuchumi:-
(a) Je, hadi sasa Serikali imechukua hatua gani ili kuongeza wanunuzi wa tumbaku ili kuleta ushindani wa bei na kuwa na masoko ya uhakika?
(b) Je, Serikali imechukua hatua gani kuondoa tozo na makato lukuki katika bei ya tumbaku?
(c) Je, Serikali imechukua hatua gani katika kupunguza daraja za tumbaku?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nasi kama Wizara tunatambua kwamba Mheshimiwa Margaret Sitta amekuwa mshauri mkubwa sana, lakini vile vile amesimamia suala la tumbaku nasi tunapenda kutoa pole kwa msiba mkubwa uliompata.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hapa nchini yapo makampuni machache yanayojishughulisha na biashara ya tumbaku, hivi sasa Serikali kupitia Bodi ya Tumbaku inaendelea kutafuta masoko zaidi ili kuongeza uzalishaji na ushindani wa bei. Hadi sasa Kampuni ya China Sunshine inakamilisha taratibu za kuingiza tumbaku yetu katika soko la China. Vile vile imefanikiwa kupata Kampuni ya Sino Cigarette ya China ambayo inatarajia kununua tumbaku ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, Bodi imeshaisajili Kampuni hiyo na kuiruhusu kufanya maandalizi ya ununuzi wa tumbaku. Pamoja na hayo, Soko la Tumbaku Duniani lipo kwenye kampuni kubwa chache zinazofanya biashara, siyo kwa ushindani, bali ni muungano wa ukiritimba (cartel) katika kupanga bei na kiasi cha kununua kutoka nchi fulani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, pamoja na kuwa ushindani ni mojawapo ya vigezo vya kupata bei nzuri, lakini katika zao la tumbaku vipo vigezo vingine vya kuwezesha kupata bei nzuri, ambavyo ni pamoja na ubora, vigezo vya kukubalika sokoni (compliance) na ufanisi katika uendelezaji wa Vyama na Biashara yenyewe katika maana ya efficiency. Hivi sasa Serikali inaelekeza nguvu kwenye kuwezesha zao kukubalika sokoni kwa kuboresha uhifadhi wa mazingira, kuondoa ajira ya watoto na kuongeza ufanisi kwa kuimarisha Vyama vya Ushirika, mazingira ya kufanyia biashara, kuondoa tozo, kodi na gharama za uzalishaji zisizo za lazima.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Wizara zinazohusika inafanyia mapitio tozo na kodi zilizopo katika mazao mbalimbali ikiwemo zao la tumbaku ili kuona uwezekano wa kuziondoa au kuzipunguza. Uchambuzi huo utakamilika kabla ya Bajeti ya Serikali ya mwaka 2017/2018 ambapo tunategemea kuwepo kwa unafuu mkubwa katika makato mbalimbali katika zao la tumbaku na mazao mengine.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Bodi kwa kushirikiana na wadau wa tasnia ya tumbaku imepunguza madaraja 10 na hivi sasa kuna madaraja 62 badala ya 72 ambayo yatatumika msimu huu wa kilimo katika maana ya 2016/2017. Aidha, wakulima wanashauriwa kuongeza ubora wa tumbaku wanayozalisha jambo ambalo litapunguza madaraja moja kwa moja.
MHE. MARGARET S. SITTA Aliuliza:-
Pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kutatua matatizo ya wakulima wa tumbaku katika Mkoa wa Tabora akiwemo wa Wilaya ya Urambo.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuunda Bodi ya Tumbaku (TTB) nyingine ili ianze kazi haraka iwezekanavyo baada ya Bodi ya Tumbaku iliyovunjwa?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha pembejeo za msimu ujao zinamfikia mkulima wa tumbaku mapema wakati huu ambapo bodi husika imevunjwa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI Alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa
Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, lenye Sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, A, ni kweli kuwa Serikali imevunja Bodi ya Tumbaku Tanzania kwa lengo la kufanya marekebisho katika utendaji kazi wa bodi. Hatua hii ya kuvunja Bodi ya Wakurugenzi haihusu kusitisha shughuli zinazotekelezwa katika tasnia hii ya tumbaku kwani wapo wataalam wanaoendeleza utekelezaji wa mpango uliopo na kuendeleza soko la tumbaku nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia umuhimu wa uwepo wa Bodi ya Tumbaku nchini kwa maendeleo ya tasnia hii ya tumbaku, utaratibu unaandaliwa wa kuunda Bodi mpya ya Wakurugenzi haraka iwezekanavyo na wananchi watataarifiwa kupitia tamko la Serikali mara baada ya taratibu kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pembejeo za muhimu kwenye zao la tumbaku ni pamoja na mbolea aina ya NPK, mbolea aina ya CAN, nyuzi za kufungia tumbaku wakati wa kuvuna na wakati wa masoko, vipande vya magunia na madawa. Pembejeo hizo huagizwa kupitia vyama vikuu vya ushirika kwa kila eneo kwa kupitia mchakato wa zabuni unaosimamiwa na kuratibiwa na vyama vikuu vya ushirika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kuwa wakulima wanahitaji huduma muda wote hasa kipindi hiki cha kuelekea masoko ya tumbaku kwa msimu wa 2017/2018, Serikali kupitia Mrajisi wa Vyama vya Ushirika nchini ameshateuwa timu nyingine ambayo ipo Mkoani Tabora ikiendelea kuratibu na kusimamia masuala mbalimbali ya wakulima, ikiwa ni pamoja na kuandaa upatikanaji wa pembejeo kwa msimu ujao. Hivyo, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa, pamoja na Bodi ya WETCU kuvunjwa, lakini kazi za chama kikuu zinaendelea kama
kawaida.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA (K.n.y. MHE. MARGARET S. SITTA) aliuliza:-
Kwa mujibu wa takwimu za Serikali kumekuwa na ongezeko kubwa la Taasisi za Elimu zikiwemo shule za Serikali na zisizo za Serikali za msingi na sekondari, shule maalum, vyuo vya ualimu na vituo vya elimu ya watu wazima; na kwa kuwa suala la ubora wa elimu ni kipaumbele kwa Watanzania walio wengi.
Je, kwa nini Serikali isiunde chombo kinachojitegemea
cha ukaguzi wa elimu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya Ukaguzi wa Shule iliundwa kwa mujibu wa Sheria ya Elimu Sura ya 353 ya sheria za nchi ikiwa na jukumu ka kufuatilia ubora wa elimu ya msingi, sekondari na vyuo vya ualimu kwa kuzingatia viwango vya utoaji wa elimu vilivyowekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Idara ya ukaguzi wa shule ilianzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Elimu, kwa sasa wizara yangu inafanya mabadiliko ya sheria ya mfumo mzima wa elimu ili iende sambamba na Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014. Suala la ukaguzi wa shule kuwa chombo kinachojitegemea litaangaliwa kwa mapana katika hatua za kufanya mabadiliko ya sheria hiyo, pamoja na nyingine ambazo zitaweza kuongeza ufanisi katika ukaguzi wa shule.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Wilaya ya Urambo inapokea umeme kutoka kwenye kituo cha kupoozea umeme cha Kaloleni umbali wa kilometa 90 kufika Urambo ambako ndiko kiliko kikata umeme inapokuwa kumetokea tatizo katika njia. Aidha, chanzo hicho cha umeme pia kimetegemewa na Wilaya ya Kaliua, Jimbo la Ulyankulu na vijiji vya Ikomwa, Igange, Tumbi, Ilolangulu hadi Ugoola (Tabora na Uyui); uzoefu unaonyesha kwamba kama kukitokea tatizo la kiufundi katika njia huwa inasababisha kukatika kwa umeme katika njia nzima likiwemo Jimbo la Urambo na kusababisha malalamiko mengi kwa TANESCO.
Je, kwa nini Serikali isijenge kituo cha kupoozea umeme (substation) karibu na Wilaya ya Urambo ili kiweze kutoa umeme wa uhakika katika Wilaya hiyo inayozidi kukua katika mahitaji ya umeme hasa katika kutekeleza sera ya viwanda na katika taasisi zinazotoa huduma za kijamii kama hospitali, shule na kadhalika kwenye Jimbo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inaendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mikoa ya Tabora na Kigoma kwa kujenga njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 133 yenye urefu wa kilometa 372 kutoka Tabora kupitia Urambo, Kaliua, Uvinza na hatimaye Kigoma.
Mheshimiwa Spika, katika mradi huu, kituo cha kupoza umeme (substation) cha kilovoti 132 kitajengwa kati ya Urambo na Kaliua kitakachosafirisha umeme katika Wilaya ya Urambo, Kaliua, Uvinza hadi Kigoma na hivyo kuimarisha miundombinu katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, upembuzi yakinifu wa mradi huu ulianza mwezi Juni, 2017 na utakamilika mwezi Septemba, 2017. Ujenzi rasmi wa mradi unatarajiwa kuanzia mwezi Aprili, 2018 na kukamilika mwezi Agosti, 2018. Mradi huu utagharimu shilingi bilioni 179.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Tatizo la uhaba wa watumishi wa Idara ya Afya Urambo linaathiri utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.
(a) Je, Serikali inachukua hatua gani za dharura katika kuliondoa tatizo la uhaba wa watumishi wa Idara ya Afya Wilayani Urambo?
(b) Je, Serikali inaweza kuchukua vijana wa Urambo na kuwapeleka vyuoni kusoma kwa makubaliano ya kurudi kufanya kazi Urambo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE)alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ina upungufu wa watumishi wa kada ya afya. Tatizo hili linazikabili Halmashauri nyingi nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa na utaratibu wa kuwaajiri wataalam wa kada ya afya kipindi wanapohitimu mafunzo na kufaulu vizuri katika masomo yao. Aidha, kuanzia mwezi Novemba, 2015 Serikali ilisitisha zoezi la kuajiri ili kubaini watumishi wa umma walioajiriwa na hawakuwa na sifa stahiki na kuwatambua watumishi halali.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukamilisha zoezi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma imeendelea kutoa vibali vya watumishi wa kada za afya ambapo mwezi Aprili, 2017 tulipata kibali cha kuajiri madakrati 209. Katika kibali hicho, Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ilipata madaktari wawili. Vilevile mwezi Julai, 2017 tumepokea kibali cha watumsihi 2,152 ambao wamepangiwa katika Mikao na Halmashauri kwa uwiano ili kupunguza uhaba wa watumishi. Katika mgao huu Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ilipata watumishi 17. Serikali itaendelea kupanga watumishi kwa kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa kuwasomesha vijana kwa makubaliano ya kurudi kufanyakazi umeshindwa kufanikiwa kwani uzoefu unaonesha vijana wengi wamesomeshwa na kuhitimu wanakuwa wamebadili mawazo na kuamua kufanyakazi sehemu nyingine na kuacha mgogoro kati ya wasomeshaji na aliyesomeshwa. Serikali inaendelea kuboresha mazingira kama vile upatikanaji wa nyumba pamoja na huduma za kijamii ili kuwafanya watumishi wanaoajiriwa waweze kubakia katika maeneo waliyopangwa.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Kumekuwa na mgogoro wa mipaka katika Pori la Hifadhi ya North Ugala, Wilayani Urambo, Kata ya Nsenda, Kijiji cha Kangome, Kitongoji cha Lunyeta. Mgogoro huo umesababishwa na mipaka mipya iliyowekwa na hivyo kusababisha upungufu wa eneo la shughuli za kilimo na ufugaji.
(a) Je, Serikali inafahamu kuwepo wa mipaka ya zamani ambayo haikuzingatiwa wakati wa kuweka mipaka mipya?
(b) Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa mipaka ili wananchi wapate eneo la kutosha kwa ajili ya kilimo na ufugaji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo lenye sehemu
(a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu wa Hifadhi ya North Ugala unapatikana katika Wilaya za Urambo na Kaliua. Msitu huu unaomilikiwa na Serikali Kuu chini ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania na una ukubwa wa hekta 163,482.39 na ulianzishwa rasmi 1956 na kuchorewa ramani ya JB Namba 307 ya tarehe 22/10/1956.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu wa North Ugala umehifadhiwa kutokana na umuhimu wake hasa katika kuhifadhi vyanzo vya maji, mapito (shoroba) za wanyamapori hasa wanapohama kutoka katika Mapori ya Akiba ya Kigosi, Ugala na Rungwa kuelekea Pori la Akiba la Rukwa, Lukwati hadi Hifadhi ya Taifa ya Katavi iliyopo Mkoani Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, hifadhi hii inatumika katika uzalishaji na uvunaji wa mazao ya misitu ikiwemo asali, nta, mbao na mkaa. Serikali iliagiza kuweka vigingi kwenye mipaka yote ya Hifadhi za Taifa, misitu, mapori ya akiba na tengefu. Katika hifadhi ya msitu wa North Ugala, vigingi viliwekwa na baadae kuwaondoa wananchi wote waliokuwa wamevamia hifadhi hiyo. Baada ya kupitia na kuweka vigingi katika mpaka, ilionekana kwamba mpaka umenyooka kutoka kigingi namba 5 hadi 6 na kupitia katika mpaka wa vijiji vya Izengabatogilwe, Isongwa, Azimio, Mtakuja, Ifuta, Utenge, Tumaini, Kamalendi, Igombe, Zugimlole na Uyumbu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mpaka mpya uliowekwa bali vigingi viliwekwa kwa mujibu wa GN iliyounda hifadhi hiyo. Ili kumaliza migogoro kati ya hifadhi na wananchi wanaopakana na hifadhi ya misitu; Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa misitu, ushirikishwaji wa wananchi katika uhifadhi, kuimarisha mipaka kwa kuweka vigingi na mabango ya tahadhari, kupanda miti mipakani, kushirikiana na sekta nyingine katika kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi na kuhamasisha ufugaji na kilimo cha kisasa. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Pamoja na kuishukuru Serikali kwa hatua mbalimbali zilizochukuliwa katika kumwondolea mkulima matatizo ya zao la tumbaku:-
• Je, Serikali imechukua hatua zipi katika kuimarisha utendaji kazi wa Bodi mpya ya Tumbaku ili ifanye kazi kikamilifu?
• Je, Serikali inawahakikishiaje wakulima wa tumbaku upatikanaji wa mbolea kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Bodi ya Wakurugenzi wa Bodi ya Tumbaku Tanzania ilizinduliwa rasmi tarehe Mosi Disemba, 2017. Ili kuimarisha utendaji kazi wake kikamilifu, Serikali imeiagiza kuwa tumbaku iendelee kuwa miongozi mwa mazao mkuu yanayowanufaisha wakulima ili kuliingizia Taifa fedha za kigeni kwa kuhakikisha kuwa ubora wa tumbaku unaongezeka kwa asilimia 15 ifikapo mwaka 2021 na uzalishaji wake kufikia tani laki moja na ishirini kutoka tani elfu sitini na tatu za sasa.
Mheshimiwa Spika, tumbaku inazalishwa kwa mujibu wa sheria na taratibu na wakulima wanazalisha kwa mkataba ili kuwa na soko la uhakika.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tumbaku ni moja ya zao la kimkakati, Bodi imelekezwa kuyataka makampuni ya ununuzi kufanga mikataba na Bodi ya Tumbaku Tanzania na kisha kuyapangia maeneo ya kwenda kununua badala ya utaratibu wa sasa ambapo makampuni hujichagulia maeneo ya kwenda kununua.
Mheshimiwa Spika, hatua nyingine ni kutafiti na kubaini aina nzuri za tumbaku zinazopendwa na wanunuzi ili zilimwe na kuwauzia wanunuzi wa aina hizo za tumbaku; kuwachukulia hatua za kinidhani watendaji wasiowajibika kikamilifu na kufuata vizuri kalenda ya uzalishaji wa tumbaku.
(b) Mheshimiwa Spika, katika msimu wa mwaka wa 2017/2018, mbolea ya tumbaku ilichelewa kutokana na kuchelewa kwa maafikiano ya bei ya kununulia tumbaku ambayo ni kigezo kwa kila kampuni kuahidi kiasi cha tumbaku itakachonunua na hivyo kubaini kiasi cha mbolea itakayotumika kuzalisha kiasi hicho cha tumbaku.
Mheshimiwa Spika, ili mbolea ianze kuagizwa maafikiano ya bei yanatakiwa kukamilika kati ya Machi na Mei kila mwaka. Katika msimu wa kilimo wa 2018/2019, Bodi ya Tumbaku Tanzania inaendelea kuratibu majadiliano ya bei kati ya wanunuzi na wakulima ili uagizaji wa mbolea ufanyike mapema. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Serikali imeanzisha Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC)
kwa lengo la kutatua matatizo ya walimu.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha Tume hiyo ili ifanye kazi kikamilifu kama ilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) imeanzishwa kwa Sheria ya Utumishi wa Walimu Namba 25 ya mwaka 2015 na kuanza kutekeleza majukumu yake rasmi tarehe 1Julai, 2016 kupitia Ofisi za Tume zilizopo katika Wilaya 139 za kiutawala ambazo zinasimamiwa na Makatibu Wasaidizi wa Wilaya. Majukumu ya tume yameainishwa katika kifungu cha 5 cha Sheria hiyo ambayo ni pamoja na kusimamia mikataba ya ajira za walimu, kuwapandisha madaraja na kuchukua hatua za kinidhamu, ikiwemo kusikiliza rufaa kutoka ngazi za chini, kuwatambua na kutunza kumbukumbu za walimu wa shule za msingi na sekondari, kusimamia mafunzo ya walimu walio kazini, kufanya tafiti mbalimbali zinazohusu utumishi wa walimu na kutathmini hali ya utumishi wa walimu na kusimamia maadili ya utumishi wa walimu.
Mheshimiwa Spika, huu ni mwaka wa pili tu wa uhai wa Tume hiyo ambayo bado ni changa. Mikakati mahususi ya Serikali ili kuiimarisha zaidi Tume hiyo ni ifuatayo:-
• Kuendelea kuipatia fedha ili iweze kutimiza majukumu yake ipasavyo. Mfano katika mwaka wa fedha 2018/2019 Bunge limeiidhinishia Tume ya Utumishi wa Walimu shilingi 12,515,260,520 kati ya hizo shilingi 7,893,115,025 ni za mshahara na shilingi 4,622,145,495 ni za matumizi mengineyo, ili Tume ipate vitendea kazi kama magari, samani za ofisi na pia kugharamia vikao vya mashauri ya nidhamu na vifaa.
• Kuipatia ofisi na watumishi wa kudumu, mfano, hadi sasa inao Makatibu Wasaidizi wa Wilaya 138 ambao wameshajengewa uwezo na mwaka ujao 2018/2019 wataajiriwa watumishi 45 wapya na wengine 145 watahamishiwa kwenye Tume kama uhamisho wa kawaida. Uimarishaji wa Tume hiyo utaendelea kufanyika ndani ya wigo wa sheria iliyoanzisha Tume hiyo.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Wananchi wanaoishi katika maeneo yanayopakana na hifadhi za misitu katika Wilaya ya Urambo wamepitia migogoro mingi ya mipaka na hata kuchomewa nyumba na mali:-
Je, ni lini Serikali itamaliza migogoro ya mipaka katika Kata za Nsenda, Uyumbu na Ukondamayo ili wananchi waendelee na kilimo pamoja na shughuli nyingine za kuwaletea maendeleo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Nsenda na Ukondamoyo ni mojawapo ya kata zinazopakana na Msitu wa Hifadhi wa North Ugalla. Msitu wa Hifadhi wa North Ugalla ulitengwa mwaka 1956 ukiwa na hekta 278,423.3 na kusajiliwa kwa ramani namba 307 chini ya Wilaya ya Tabora. Mwaka 2008 eneo la mpaka wa kaskazini mwa msitu ulipunguzwa kwa zaidi ya umbali wa kilomita tano, sawa na eneo la hekta 114,940.91 kwa ajili ya matumizi ya wananchi. Hivyo, mwaka 2008 eneo la msitu wa North Ugalla lililobaki ni hekta 163,482.39 kwa ramani 2,567 iliyosajiliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu huu umehifadhiwa kwa madhumuni ya kutunza ardhi na udongo eneo la lindimaji (catchment area), kuhifadhi bioanuai, kurekebisha hali ya hewa, kuzalisha mazao ya timbao na yasiyo ya timbao kwa ajili ya kutumiwa kwa utaratibu maalum.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2014, wananchi waliovamia msitu huo waliondolewa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Namba 14 ya mwaka 2002. Hatua zilizochukuliwa za kuondoa migogoro ya mipaka kati ya Vijiji vya Kata za Nsenda na Ukondamoyo ilikuwa; kwanza kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi ya vijiji husika. Mpango huo uliandaliwa mwaka 2017 na Serikali za Vijiji kwa kushirikiana na Mradi wa Miombo chini ya usimamizi wa Tume ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii ya kutayarisha mpango wa matumizi bora ya ardhi ilifanyika bila ya kuwa mgogoro wowote. Aidha, hati miliki za kimila zinaendelea kutolewa na elimu kuhusu usimamizi shirikishi wa misitu katika vijiji husika. Hatua hii ya utoaji wa elimu kwa wananchi juu ya kutambua, kubaini mipaka halali ya vijiji na mpaka wa hifadhi ya msitu wa North Ugalla zinafanyika kwa ushirikishaji wa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Uyumbu kuna Jumuiya ya Hifadhi ya Jamii ya Wanyamapori ya UWIMA ambayo inaundwa na Vijiji vitatu vya Izimbili, Nsogoro na Izegabatogilwe. Vijiji hivyo vilisaidiwa kutengeneza Mpango wa matumizi bora ya ardhi mwaka 2004. Mwaka 2006 mpaka 2007, baadhi ya wananchi walivamia eneo la ukanda wa malisho linalotumika kama ushoroba. Mwaka 2007 wananchi hao waliondolewa kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kijiji cha Tebhela ambao awali kilikuwa Kitongoji cha kijiji cha Nsogoro walivamia eneo hilo kwa kuweka makazi, kuendesha kilimo na malisho ya mifugo. Hivyo, tatizo lililopo ni uanzishwaji wa eneo jipya la utawala (Kijiji cha Tebhela) bila kuzingatia eneo lililopo. Hata hivyo UWIMA na Halmashauri ya Wilaya ya Urambo wamefanya mikutano kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kuheshimu mipaka ya Hifadhi ya Jamii na matumizi bora ya ardhi.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Moja kati ya changamoto zinazowakabili wakulima wa tumbaku katika Wilaya ya Urambo ni madeni yanayotokana na mikopo ya pembejeo ikiwemo mbolea:

(a) Je, Serikali inachukua hatua gani ili kuwasaidia wakulima kuepukana na changamoto hii?

(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kushusha bei ya pembejeo ili kumsaidia mkulima?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret S. Sitta, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka 2008, Serikali imeboresha mfumo wa upatikanaji wa pembejeo za zao la tumbaku kwa wakulima kupata pembejeo kupitia vyama vya ushirika tofauti na ilivyokuwa kabla ya mwaka 2008 ambapo pembejeo za tumbaku zilitolewa kupitia kampuni zinazonunua tumbaku kwa kuwakopesha wakulima na kuwakata wakati wa mauzo. Utaratibu huo ulikuwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na riba kubwa isiyo na tija kwa mkulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondokana na madeni yatokanayo na riba za mkopo wa pembejeo, Serikali imewahamasisha wakulima kupitia vyama vyao vya ushirika kuainisha mahitaji ya pembejeo mapema na wamekubali kukatwa kiasi cha fedha kutokana na mauzo ya tumbaku ili kuagiza pembejeo hizo kwa wakati. Mfano Chama cha Msingi cha Kahama (KACU) wamekubaliana kukatwa Sh.60 kwa kila kilo kwa lengo la kukusanya takribani shilingi bilioni 3 zitakazotosheleza kuagiza asilimia 75 ya mahitaji ya pembejeo. Utaratibu huo unafanyika kwa vyama vyote ambapo wakulima watanufaika kwa kupata bei ndogo kuliko ile ya kukopa.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Mfumo wa uagizaji Mbolea kwa Pamoja (Bulk Procurement System - BPS) ulianzishwa kwa lengo la kupunguza gharama au kodi kwa wakulima. Hata hivyo, mfumo huo unategemea bei ya mbolea iliyopo katika soko la dunia kwa wakati huo. Kutokana na changamoto za ongezeko la bei ya mbolea katika soko la dunia, Serikali inasimamia Mfumo wa Uagizaji wa Mbolea kwa pamoja ili kuhakikisha kuwa wakulima wakiwemo wa zao la tumbaku wanapata pembejeo kwa wakati na kwa bei nafuu.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Mgogoro wa ardhi kati ya Jeshi la magereza na wananchi wa Kata ya Ukondamayo hususan Kijiji cha Tumaini umedumu kwa muda mrefu sasa.

Je, Serikali inachukua hatua gani kutatua na kumaliza mgogoro huu?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukujulisha kwambakwa sasa hakuna mgogoro wa ardhi kati ya kata ya Ukandamoyo hususani kijiji cha Tumaini na gereza la ilimo Urambo. Ni kweli hapo awali ulikuwepo mgogoro baina vya vijiji vinne mojawapo kijiji cha tumaini, Mgogoro huo ulitatuliwa na kuhitishwa mwaka 200 kwa kuhutimishwa mwaka 2000 kwa kushirikishwa viongozi kutoka wizira ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Ardhi, Jeshi la Magereza, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Urambo na Serikali ya vijiij vyote nine vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo Kijiji cha Tumaini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hitimisho la mgogoro huo ni baada ya Jeshi la magereza kukubali kuotka eneo la jumla ya ekari 3,218 kwa vijiji vilivyokuwa na mgogoro mojawapo kijiji cha Tumaini wakapewa ekari 505, Imalamakoye ekari 195, Nsendakanoge ekari 1,655 na Itebulanda ekari 860.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha hati ya makubaliano ya hitimisho la mgogoro ilisainiwa na viongozi wa vijiji vyote vinne vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo kijiji cha Tumaini na mawe ya mipaka yaani beacons yakawekwa upya kwa utambulisho wa namba Uv 66, Uv 69, Uv 107, Uv 35 na Uv 108.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuwasaidia Wakulima nchini hususan wakulima wa tumbaku ili zao hili la biashara liweze kuwasaidia wakulima na Taifa kwa ujumla kwa kuingiza fedha za kigeni:-

(a) Je, Serikali inawahakikishiaje wakulima wa tumbaku katika Mkoa wa Tabora ikiwemo Wilaya ya Urambo kwamba mbolea itakuwepo mwezi Agosti wanapoanza kilimo cha tumbaku kulingana na makisio yao;

(b) Je, wanunuzi wangapi wamepatikana hadi sasa ili wakulima walime tumbaku nyingi kwa bei ya ushindani ili kumnufaisha Mkulima na Taifa kwa ujumla.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kwa ridha yako naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya na kwa kila jambo. Jambo la pili nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa imani aliyoionesha kwangu na imani aliyowaonesha wananchi wa Jimbo la Nzega. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, makisio ya mahitaji ya mbolea kwa Mkoa wa Tabora ni jumla ya tani 9,000 sawa na asilimia 42 ya mahitaji ya mbolea ya zao la tumbaku nchini ya tani 21,582. Kati ya kiasi hicho tani 205 za NPK ni kwa ajili ya vitalu na tani 8,887 NPK kwa ajili ya mashambani. Aidha, mahitaji ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ni jumla ya tani 2,468 ambapo tani 50.73 ni NPK kwa ajili ya vitalu, tani 1,741 ni NPK kwa ajili ya mashambani na tani 676 mbolea aina ya CAN kwa ajili ya shambani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia tarehe 15 Agosti, 2019 upatikanaji wa mbolea katika Halmashauri ya Urambo kwa ajili ya vitalu ni mifuko 1,014 sawa na upatikanaji wa asilimia 100 na usambazaji unatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba 10. Vilevile mbolea mashambani, zabuni na mikataba yote imekamilika kwa sharti kuwa mzabuni awe amekamilisha usambazaji wa mbolea hizo juma la kwanza la mwezi Oktoba, 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanunuzi wakubwa wa tumbaku hapa nchini ni kampuni za Alliance One Premium Active Japan Tanzania International leaf, Tanzania Leaf Tobacco Company Limited pamoja na kampuni ndogo ya wazalendo inayoitwa Grand Tobacco Limited. Aidha, Serikali inaendelea kufanya majadiliano ya mwisho na kampuni ya British American Tobacco ili kampuni hiyo ianze kununua Tumbaku kwa wakulima katika msimu wa mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali imeshafanya mazungumzo na nchi ya China ili iweze kununua Tumbaku kutoka Tanzania ambapo tayari nchi hiyo imeainisha aina ya mbegu za Tumbaku ambazo wanataka zizalishwe nchini ili kukidhi ladha ya Tumbaku wanayohitaji. Mbegu hizo kimsingi hazizalishwi nchini kwa sasa taratibu za kitaalamu na za kisheria zinaendelea ili aina hizo ziweze kuzalishwa nchini na kufungua fursa ya soko la China. (Makofi)
MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. MARGARET S. SITTA) aliuliza:-

(a) Je, Serikali ipo tayari kuangalia bajeti ya Hospitali ya Wilaya ya Urambo ambayo inahudumia wananchi wa maeneo ya Kaliua, Ulyankulu na maeneo ya jirani ili kuongeza uwezo wa kutoa huduma?

(b) Hospitali ya Wilaya ya Urambo ina majengo mawili ya ICU na maabara ambayo hayajakamilika tangu yalipoanza kujengwa 2011 kupitia utaratibu wa LGDG ya mradi wa ADB. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu ombi la wananchi wa Urambo la shilingi milioni 200 ambazo zinaweza kumaliza majengo hayo?

(c) e, Serikali inatoa kauli gani kuhusu kuongeza wafanyakazi angalau Manesi 12 na Wafamasia 6 kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa Hospitalini hapo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kupunguza msongamano wa wagonjwa kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo, Serikali imepanua Kituo cha Afya Ulyankulu, Kituo cha Afya Usoke na kujenga Kituo cha Afya Usoke Mlimani kwa gharama ya jumla ya shilingi bilioni 1.2. Mpango huu utasaidia kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika vituo hivyo na kupunguza idadi ya wagonjwa wanaokwenda kutibiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Urambo.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mradi wa ujenzi wa majengo ya upasuaji, ICU na maabara uliofadhiliwa na ADB haukukamilika kutokana na tatizo la kukisia chini ya kiwango gharama za ujenzi wa majengo hayo. Serikali imepanga kukamilisha ujenzi wa majengo hayo kwa kutenga fedha kupitia bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa Fedha 2018/2019, jumla ya watumishi wapya 26 wa kada ya Wauguzi, Madaktari, Maafisa Tabibu, Mtaalam wa Mionzi na Maabara walipangwa kufanya kazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Urambo. Serikali itaendelea kuajiri na kuwapanga watumishi wa kada za afya kadri watakavyokuwa wakipatikana.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Licha ya juhudi kubwa za Serikali kumsaidia Mkulima wa zao la Tumbaku, bado zipo changamoto anazokabiliana nazo ikiwemo kutopata makisio na pembejeo kwa wakati, masoko ya uhakika na wanunuzi wengi wa Tumbaku ili kuleta ushindani wa bei:-

(a) Je, Serikali ina mikakati gani ya kuondoa changamoto hizo ili Mkulima ajiendeleze kiuchumi?

(b) Je, Serikali inashirikianaje na Wakulima wa Urambo ili wawe na Kiwanda cha Tumbaku Urambo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuchukuwa hatua mbalimbali ili kuondoa changamoto kwenye tasnia ya tumbaku zinazohusiana na baadhi ya wakulima kutopata makisio ya uzalishaji, upatikanaji wa pembejeo kwa wakati na Masoko ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msimu wa kilimo wa 2019/2020 makisio ya uzalishaji wa tumbaku ya jumla ni kilo milioni 42 yalitolewa mwezi Julai na Kampuni tatu ambazo ni Alliance One, Japan Tobacco International Leaf Services na Premium Active Tanzania Limited. Kutolewa mapema kwa makisio hayo kumewezesha Vyama vya Ushirika vya Wakulima wa Tumbaku kuagiza mbolea kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya mbolea kwa zao la tumbaku nchini ni tani 14,951 za mbolea ya NPK na tani 3,000 za mbolea ya kukuzia. Mbolea yote imeshapokelewa nchini na usambazaji unaendelea kwenye Vyama vya Msingi. Kwa Wilaya ya Urambo hadi kufikia tarehe 31 Oktoba jumla ya tani 1,774 zimesambazwa kati ya mahitaji ya tani 2,160 ya mbolea sawa na asilimia 82.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha tumbaku inayozalishwa hapa nchini inapata soko la uhakika, Serikali inaendelea na mazungumzo ili kufungua soko la tumbaku katika nchi wanachama wa COMESA (Algeria, Misri na Sudan), ambao niwateja wakuu wa tumbaku ya Moshi inayozalishwa nchini. Serikali ilituma ujumbe wa wataalam watano kwenda nchi ya China kujifunza namna bora ya uzalishaji wa tumbaku inayohitajika kwa soko la China.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufutia mafunzo hayo, aina tano za mbegu za tumbaku zimeingizwa nchini kwa ajili ya kufanyiwa majaribio katika maeneo ya uzalishaji wa tumbaku nchini. Tayari majaribio kwenye jumla ya eneo la ekari 10 yanaendelea nchini chini ya usimamimizi wa Taasisi ya Utafiti wa Tumbaku (TORITA) na Bodi ya Tumbaku. Aidha, Serikali imefanya mazungumzo na Kampuni ya British American Tobacco Ltd ambayo imeonesha nia ya kununua jumla ya kilo milioni nane ya Tumbaku inayozalishwa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha kwamba wawekezaji wa tumbaku waliopo nchini wanaendelea kuongeza uwekezaji, mwezi Septemba, Wizara ya Kilimo ilikutana na Kampuni za wanunuzi wa tumbaku kwa lengo la kujadili na kupata ufumbuzi wa changamoto zilizopo. Kutokana na kikao hicho, ilikubalika kuondoa kesi zilizofunguliwa na Tume ya Ushindani na kufanya makubaliano ya kirafiki nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, matatizo yanayohusiana na sula la kodi ya VAT, mchakato wa kuweza kupitia VAT returns kwa taasisi hizo nne unaendelea; na pale ambapo madai yao ya halali yataonekana, basi Serikali itawalipa kufuatana na utaratibuwa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Urambo imetoa ekari 20 kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha kusindika tumbaku. Taratibu za umilikishwaji wa ardhi kisheria kwa ajili ya kiwanda zinakamilishwa. Aidha, Serikali itashirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Benki ya TADB na Chama Kikuu cha Ushirika cha Urambo ili kuhakikisha kuwa kiwanda hicho kinaanzishwa.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Katika Wilaya ya Urambo kulikuwa na Chuo cha Ualimu ambacho kilisaidia sana kuleta chachu ya maendeleo ya elimu na uchumi kwa wananchi wa Urambo.

(a) Je, ni sababu zipi zilizosababisha Chuo cha Ualimu Urambo kufungwa/kuhamishwa?

(b) Je, Serikali haioni iko haja ya kuangalia upya uwezekano wa kurudisha Chuo cha Ualimu Urambo?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1995 Serikali iliamua kubadilisha baadhi ya vyuo vya ualimu kuwa shule za sekondari, Urambo kikiwa kimojawapo. Uamuzi huo ulitokana na sababu zifuatazo; mahitaji makubwa ya shule za sekondari hasa katika ngazi ya kata pamoja na maamuzi ya Serikali kuhitimisha utoaji wa mafunzo ya ualimu kwa wahitimu wa darasa la saba Ualimu Daraja la Tatu B ili kuinua kiwango cha elimu na uwepo wa vyuo vingi vya ualimu ambavyo vinatosheleza mahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na sababu hizo Serikali ilikibadilisha Chuo cha Ualimu Urambo na kuanzisha Shule ya Sekondari Ukombozi ambayo ni shule ya kutwa.

Aidha, kwa kuifanya kuwa shule ya kutwa yaliyokuwa mabweni yalikarabatiwa na kubadilishwa kuwa madarasa sita na kujenga madarasa mengine sita na kuwezesha shule hiyo kudahili wanafunzi 888 ambapo idadi ya wasichana ni 426 na wavulana ni 462.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina jumla ya vyuo vya ualimu 35 vya Serikali ambavyo hudahili wanachuo kutoka nchi nzima. Kuanzia mwaka 2016/2017 Serikali imefanyia upanuzi na ukarabati mkubwa vyuo 24 katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali inaendelea kufanya ukarabati wa vyuo vingine kumi kwa lengo la kuendelea kuongeza nafasi za udahili ili kuendelea kutosheleza mahitaji ya walimu nchini.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Wilaya ya Urambo inakabiliwa na uhaba mkubwa wa maji hadi Serikali ikaingiza Wilaya hii katika mpango mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria, wakati wananchi wa Urambo wakisubiri mpango huo wa maji kutoka Ziwa Victoria:-

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi ya kuchimba visima 30 katika Wilaya ya Urambo?
WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margareth Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na uhaba wa maji, Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ilisaini Mkataba na uliokuwa Wakala wa Uchimbaji Visima (DDCA) tarehe 26 Machi, 2018 wa gharama ya Shilingi milioni 620.9 kwa ajili ya kuchimba visima 30 katika Vijiji vya Ussoke Mjini viwii; Itundu viwili; Kasisi viwili; Kiloleni viwili; Tulieni kimoja; Machinjioni kimoja; Ulassa B kimoja; Ifuta viwili; Ugalla viwili; Uyogo viwili; Nsenda viwili; Unzali viwili; Vumilia viwili; Kalembela viwili; Ussoke Mlimani viwili; Katunguru viwili; na Kapilula kimoja.

Mheshimiwa Spika, utafiti wa maeneo ya uchimbaji wa visima hivyo umekamilika na mradi huu utatekelezwa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) ambapo unatarajiwa kufanyika mwezi Mei, 2020.

Mheshimiwa Spika, vilevile, Wilaya ya Urambo kupitia Mpango wa Matokeo (PforR) imepanga kuchimba visima virefu 18 ili kupunguza tatizo la uhaba wa maji katika Vijiji vya Isongwa, Kichangani, Milambo, Ulassa A, Kamalendi, Mtakuja, Sipungu, Tumaini, Ukwanga, Itegamatwi, MotoMoto, Kalembela, Usoke Mlimani, Usoke Mjini, Itebulanda, Tebela, Kasisi na Vumilia. Utekelezaji wa kazi hiyo unatarajiwa kuanza mwezi Aprili, 2020.
MHE. MARGARET S. SITTA Aliuliza: -

Serikali imeanzisha Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla Wilayani Urambo: -

(a) Je, ni lini Serikali itatoa elimu elekezi kwa wananchi wa maeneo hayo juu ya matumizi ya eneo husika baada ya mabadiliko yaliyotokea?

(b) Kutokana na ongezeko la watu, je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wananchi maeneo kwa ajili ya ufugaji nyuki, mifugo na kilimo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Sitta, Mbunge wa Urambo lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla ina ukubwa wa kilomita za mraba 3,865. Hifadhi hii ilianzishwa kwa Azimio la Bunge la tarehe 10 Septemba, 2019 na Tangazo la Serikali Na. 936 la tarehe 29 Novemba, 2019. Hifadhi ipo katika Wilaya ya Urambo na Kaliua Mkoani Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, madhumuni ya kuanzishwa kwa hifadhi hii ni kuimarisha uhifadhi ili kuunganisha mfumo wa ikolojia wa Malagarasi - Muyowosi ambao ni ardhi oevu yenye umuhimu wa kitaifa na kimataifa pamoja na kuongeza pato la Taifa kutokana na ongezeko la idadi ya watalii, kuwezesha jamii kunufaika na fursa za utalii na kutunza vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na Mpango kutoa Elimu ya Uhifadhi ambao unalenga kujenga uwezo na uelewa kwa wananchi, viongozi na wadau wengine wa uhifadhi ambao wanapakana na Hifadhi za Taifa. Utekelezaji wa mpango huo, ulianzia kwenye Wilaya ya Kaliua, ambapo ulihusisha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya na vijiji 12. Hatua inayofuatia ni kuendelea na programu hiyo kwenye Wilaya ya Urambo, ambapo zoezi litaanzia kwenye Kata ya Nsendo ambako vijiji nane (8) vitahusishwa. Nia kubwa ya uhamasishaji huo ni kujenga uelewa kuhusu sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa Hifadhi za Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka 2021/2022, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuendelea kutekeleza mpango wa kutoa elimu ya uhifadhi na kuweka mkazo kwenye kuandaa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya husika, pamoja na Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi; kuendelea kuhakiki mipaka ya maeneo ya hifadhi kwa kuweka alama za kudumu na mabango elekezi ili mipaka ionekane kwa urahisi; na kuendelea kutoa huduma za ugani kwa ushirikiano na wadau wa uhifadhi katika maeneo mbalimbali ili kutunza mazingira, vyanzo vya maji na misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 6 (1) cha Sheria ya Hifadhi za Taifa Tanzania, Sura 282 iliyofanyiwa Mapitio mwaka, 2002 kinabainisha kuwa Mheshimiwa Rais akishatangaza eneo la ardhi yoyote kuwa Hifadhi ya Taifa, haki zote za awali zikiwemo hati miliki zilizokuwa juu ya eneo husika zinakoma. Wizara yangu itawasiliana na Mamlaka za Mikoa na Halmashauri ili kupata maeneo nje ya Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla kwa ajili ya shughuli za ufugaji nyuki, mifugo na kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe wito kwa wananchi wote wanaozunguka Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuzuia na kupambana na ujangili na hatimaye kuboresha utalii kwa ajili ya maendeleo endelevu katika jamii husika na nchi kwa ujumla.
MHE. MARGARET S. SITTA Aliuliza:-

Serikali iliahidi kufikisha Urambo maji ya Ziwa Victoria na kwa sasa yameshafika Tabora:-

(a) Je, ni hatua zipi zimechukuliwa katika kutekeleza azma hiyo?

(b) Je, ni kiasi gani cha fedha kimetengwa katika mwaka huu wa fedha na ni lini maji yatafikishwa Urambo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepata mkopo kutoka Serikali ya India kupitia Benki ya Exim ya India ambapo jumla ya Dola za Marekani milioni 500 zitatumika kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji katika miji 28 Tanzania Bara na Zanzibar. Kupitia mkopo huo, Mji wa Urambo ni kati ya maeneo yatakayonufaika na mkopo huo. Kwa sasa utekelezaji wa mradi huo upo katika hatua za manunuzi ya wakandarasi wanaotarajiwa kuwepo eneo la miradi ifikapo Mei, 2021 na utekelezaji wake ni muda wa miezi 24.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 1.89 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji katika Halmashauri ya Urambo.
MHE. MARGARET S. SITTA Aliuliza: -

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwezesha kampuni za wazawa ili ziwalipe wakulima mara wanaponunua Tumbaku?

(b) Suala la kupata wanunuzi zaidi wa kununua tumbaku ni la muda mrefu; je kuna mafanikio yaliyopatikana?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mama Margaret Simwanza Sitta Mbunge wa Jimbo la Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu biashara ya tumbaku imekuwa ikiendeshwa bila kampuni za kizawa kushiriki katika biashara ya Tumbaku na kampuni za nje pekee ndizo zilikua zinashiriki katika biashara ya tumbaku. Wakati wa ununuzi wa tumbaku kupitia kampuni za nje ununuzi wa tumbaku ulishuka hadi kufikia tani 42,000 za mkataba na baada ya kampuni za wazawa kuingia katika ununuzi wa uzalishaji umeongeza kufikia tani 68,571 za tumbaku kupitia kilimo cha mkataba. Katika masoko ya tumbaku ya msimu wa kilimo 2020/2021 jumla ya kampuni tisa zinanunua tumbaku ya wakulima zikiwemo kampuni saba za wazawa. Hata hivyo, Kampuni hizo zimekuwa zikikabiliwa na changamoto ya kupata mitaji ya kutosha hali inayosabisha kuchelewa kuwalipa baadhi ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, katika kutatua changamoto hiyo, Mwezi Mei, 2021 Wizara ya Kilimo ilikutanisha kampuni za wazawa na taasisi za fedha kwa lengo la kukubaliana masharti nafuu yatakayowezesha kampuni hizo kupata mikopo kwa riba nafuu. Mafanikio ya majadiliano hayo yameanza kupatikana ambapo benki ya CRDB imeridhia kuzikopesha kampuni mbili za Mo Green International na Magefa Growers Limited. Aidha, Serikali inaendelea kushirikiana na kampuni za ununuzi wa tumbaku na taasisi za fedha katika kutatua changamoto ya fedha.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta soko la tumbaku katika nchi mbalimbali hasa nchi za Uarabuni, Afrika na Ulaya. Katika msimu 2020/2021 nchi yetu imefanikiwa kupata masoko mapya kwa kuuza tumbaku kwa majaribio katika nchi ya Romania, Poland na Uturuki. Aidha, sampuli za tumbaku zimetumwa nchini China na Korea Kusini kwa ajili ya masoko hayo. Juhudi za kuirejesha kampuni ya TLTC zinaendelea na mwishoni mwa mwezi Septemba 2021 Wizara itakutana uongozi wa kampuni hiyo.

Mheshimiwa Spika, ni muhimu kama nchi kuendelea kulea makampuni ya wazawa ili yawe na uwezo wa kununua tumbaku kama makampuni ya kigeni yanavyounganisha na taasisi za fedha.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Hospitali ya Wilaya ya Urambo ilijengwa mwaka 1975.

(a) Je, Serikali iko tayari kuifanyia ukarabati wa majengo na miundombinu yake yote?

(b) Je, ni lini Serikali itabadilisha mashine ya X-ray ya Hospitali hiyo ambayo imepitwa na wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa Hospitali ya Halmashauri ya Urambo ni kongwe na kwamba Serikali itafanya tathmini ya hali ya uchakavu wa miundombinu ya hospitali hiyo ili kuona namna bora ya kufanya ukarabati au ujenzi wa hospitali mpya ya halmashauri hiyo. Aidha, katika mwaka 2015 hadi 2020 Serikali imetoa shilingi milioni 413 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo. Ukarabati huo ulihusisha Wodi Maalum ya daraja la pili, ujenzi wa jengo la upasuaji, ukarabati wa mfumo wa maji taka pamoja na ukarabati wa Wodi ya Wanawake na jengo la wagonjwa wa nje na upo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji/ ukamilishaji.

(b) Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa mashine ya X- ray iliyopo katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Urambo ni ya zamani . Ni vema Halmashauri ya Wilaya ya Urambo itoe kipaumbele na kutenga fedha kupitia mapato yake ya ndani ili kununua mashine ya kisasa ya X-ray. Aidha, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, inasimamia utaratibu mpya wa Vifaa na Vifaa Tiba unaojulikana kama Managed Equipment Services (MES) kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD). Chini ya utaratibu huo, Halmashauri zinafungiwa mashine za X-ray, kupatiwa mafunzo kwa wataalam kuhusu matumizi na utunzaji wa mashine hizo, huduma ya kinga na ukarabati kwa vifaa tiba (Planned Preventive Maintenance) kwa muda wa miaka mitano. Gharama ya kununua mashine ya x-ray kwa fedha taslimu ni shilingi milioni 393.40. Endapo halmashauri itaamua kununua mashine hiyo kwa mkopo, italipa kidogo kidogo kiasi cha shilingi milioni 19.67 kila baada ya miezi mitatu kwa muda wa miaka mitano.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani kutatua mgogoro wa mipaka kati ya Jeshi la Magereza na wananchi wa Kata ya Ukondamayo hususan Kijiji cha Tumaini, Wilayani Urambo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, napenda kukujulisha kwamba kwa sasa hakuna mgogoro wa ardhi kati ya Kata ya Ukondamoyo hususani Kijiji cha Tumaini na Gereza la Kilimo Urambo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli hapo awali ulikuwepo mgogoro baina ya vijiji vinne mojawapo Kijiji cha Tumaini. Mgogoro huo ulitatuliwa na kuhitimishwa mwaka 2000 kwa kushirikishwa viongozi kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Ardhi, Jeshi la Magereza, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Urambo na Serikali ya vijiji vyote vinne vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo Kijiji cha Tumaini.

Mheshimiwa Spika, hitimisho la mgogoro huo ni baada ya Jeshi la Magereza kukubali kutoa eneo la jumla ya ekari 3,218 kwa vijiji vilivyokuwa na mgogoro mojawapo Kijiji cha Tumaini kupewa ekari 505, Kijiji cha Imalamakoye ekari 195, Kijiji cha Nsendakanoge ekari 1,655 na Kijiji cha Itebulanda ekari 860.

Mheshimiwa Spika, aidha, hati ya makubaliano ya hitimisho la mgogoro ilisainiwa na viongozi wa vijiji vyote vinne vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo Kijiji cha Tumaini na mawe ya mipaka (beacons) yakawekwa upya kwa utambulisho wa Namba Uv 66, Uv 69, Uv 107, Uv 35 na Uv 108, nakushukuru.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani kutatua mgogoro wa mipaka kati ya Jeshi la Magereza na wananchi wa Kata ya Ukondamayo hususan Kijiji cha Tumaini, Wilayani Urambo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, napenda kukujulisha kwamba kwa sasa hakuna mgogoro wa ardhi kati ya Kata ya Ukondamoyo hususani Kijiji cha Tumaini na Gereza la Kilimo Urambo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli hapo awali ulikuwepo mgogoro baina ya vijiji vinne mojawapo Kijiji cha Tumaini. Mgogoro huo ulitatuliwa na kuhitimishwa mwaka 2000 kwa kushirikishwa viongozi kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Ardhi, Jeshi la Magereza, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Urambo na Serikali ya vijiji vyote vinne vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo Kijiji cha Tumaini.

Mheshimiwa Spika, hitimisho la mgogoro huo ni baada ya Jeshi la Magereza kukubali kutoa eneo la jumla ya ekari 3,218 kwa vijiji vilivyokuwa na mgogoro mojawapo Kijiji cha Tumaini kupewa ekari 505, Kijiji cha Imalamakoye ekari 195, Kijiji cha Nsendakanoge ekari 1,655 na Kijiji cha Itebulanda ekari 860.

Mheshimiwa Spika, aidha, hati ya makubaliano ya hitimisho la mgogoro ilisainiwa na viongozi wa vijiji vyote vinne vilivyokuwa na mgogoro kikiwemo Kijiji cha Tumaini na mawe ya mipaka (beacons) yakawekwa upya kwa utambulisho wa Namba Uv 66, Uv 69, Uv 107, Uv 35 na Uv 108, nakushukuru.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Je, ni lini Kata 16 zisizo na mawasiliano ya simu katika Wilaya ya Urambo zitapatiwa mawasiliano ya simu na kuwaondolea wananchi adha ya kutokuwa na mawasiliano kwa muda mrefu?

Je, ni kwa nini kuna maeneo yenye minara ya mawasiliano ya simu lakini kuna matatizo ya mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Urambo lina jumla ya Kata 18 ambapo Kata zote zina huduma ya mawasiliano isipokuwa vijiji baadhi katika Kata Tisa za Kiloleni, Itundu, Imalamakoye, Ugalla, Vumilia, Nsondo na Uyogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Utundu na Ukondamoyo zitafikishiwa huduma za mawasiliano na kampuni ya simu ya Vodacom ifikapo Oktoba, 2021, Kata za Nsondo na Uyogo zitafikishiwa huduma za mawasiliano na kampuni ya Airtel ifikapo Oktoba, 2021, Kata ya Vumilia itafikishiwa huduma za mawasiliano kupitia kampuni ya simu ya Halotel ifikapo Septemba, 2021 pamoja na Kata ya Ugala itakayofikishiwa huduma na kampuni ya simu ya TTCL ifikapo Septemba, 2021. Aidha Kata za Kiloleni na Imalamakoye zitaingizwa kwenye miradi ya mfuko itakayotekelezwa kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sababu mbalimbali zinazoweza kusababisha kukosekana huduma ya mawasiliano kwenye maeneo yenye minara ya simu ikiwa ni pamoja na hali ya kijiografia ya eneo husika kama vile uwepo wa milima, mabonde na uoto wa asili wenye miti mirefu ambayo huzuia huduma za mawasiliano. Hali ya kukosekana kwa nishati ya umeme wa uhakika pia inaweza kusababisha minara kushindwa kutoa huduma za mawasiliano. Ahsante.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

(a) Je, ni lini Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria Wilaya ya Urambo utaanza ili kutatua tatizo la maji katika Wilaya hiyo?

(b) Je, ni lini Serikali itachimba mabwawa katika Kata za Uyumbu na Kalemela hasa ikizingatiwa kuwa maombi yalishawasilishwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa huduma ya maji katika Wilaya ya Urambo ni wastani wa asilimia 40. Katika kuboresha huduma hiyo, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 inatekeleza miradi ya Itibulanda na upanuzi wa mradi kutoka Itibulanda kwenda Nsenga. Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa matanki mawili yenye ujazo wa lita 50,000, vituo 13 vya kuchotea maji na ulazaji wa mabomba umbali wa kilometa 17.6. Miradi hiyo itaongeza uzalishaji maji wa lita 32,000 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuboresha huduma ya maji katika Kata za Uyumbu na Muungano, Serikali imepanga kujenga mabwawa mawili ya Kilemela kata ya Muungano na Izimbili kata ya Uyumbu. Mabwawa hayo yatahudumia jumla ya vijiji vya 22 na mkandarasi wa ujenzi wa bwawa la Kilemela atapatikana mwezi Aprili, 2022 Kwa upande wa bwawa la Izimbili kazi ya usanifu inaendelea na itakamilika mwezi Juni, 2022. Ujenzi wa mabwawa hayo utafanyika katika mwaka wa fedha 2022/2023.

Aidha, Mji wa Wilaya ya Urambo unatarajiwa kupata huduma ya maji kupitia Mradi wa Kuboresha Huduma ya Maji katika Miji 28 ambapo chanzo cha maji kitakachotumika ni Ziwa Victoria. Taratibu za upatikanaji wa wakandarasi zimekamilika mwezi Desemba, 2021 hivyo utekelezaji utaanza ndani ya mwaka wa fedha 2021/2022.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, ni kwa nini wakulima wasianze kujua bei ya kuuzia tumbaku na bei ya pembejeo kabla ya kufunga mkataba wa uzalishaji?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Tasnia ya Tumbaku Na. 24 ya mwaka 2001 na marekebisho yake ya mwaka 2009 na kanuni za mwaka 2011, wakulima wa tumbaku wanapaswa kufunga mikataba ya uzalishaji wakiwa wanajua bei ya kuuzia tumbaku na bei ya pembejeo za kilimo. Huu ndio utaratibu uliopo unaoendelea kusimamiwa na Serikali kupitia Bodi ya Tumbaku Tanzania. Katika msimu wa mwaka 2022/2023, tayari wakulima wamepata bei ya tumbaku na pembejeo tangu tarehe 30 Agosti, 2022. Kutokana na masoko yaliyopatikana bei elekezi imepanda kutoka Dola za Marekani 1.65 mwaka 2021/2022 hadi Dola za Marekani mbili mwaka 2022/2023 kwa kilo ya tumbaku, sawa na ongezeko la asilimia 21.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itabadilisha Sera ya Chanjo kitaifa ili kuwakinga watu wengi zaidi badala ya kutibu mtu aliye na ugonjwa tayari?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa, gharama za kutibu ugonjwa wowote ni kubwa zaidi kuliko gharama za Kinga kupitia chanjo, kwa magonjwa yanayozulika kwa chanjo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali imelifanyia kazi suala hilo kwa kupitia Sheria ya Afya ya Jamii ya Mwaka 2009 kifungu 19 ambapo inawataka wazazi na walezi kuhakikisha Watoto chini ya mwaka mmoja na wajawazito wanapatiwa chanjo ili kuwakinga na magonjwa yanayozuilika na chanjo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutoa wito kwa wazazi, walezi na wajawazito kuhakikisha wanafika vituo vya kutolea huduma za afya ili kupatiwa chanjo.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, Serikali ina taarifa gani juu ya Madini yanayopatikana Wilaya ya Urambo na lini itawasaidia Wananchi ili wanufaike na Madini hayo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa tafiti zilizowahi kufanywa na GST kuhusu madini yapatikanayo nchini, Wilaya ya Urambo ina madini mbalimbali lakini ni kidogo sana. Madini hayo ni kama vile dhahabu, urani, shaba, malbo, udongo mfinyanzi au clay na miamba migumu ya ujenzi mfano granite. Pamoja na Wilaya hiyo kuwa na kiwango kidogo cha madini kwa tafiti zilizokwishafanyika, zipo leseni Nne (04) za uchimbaji mdogo. Lakini katika leseni hizo, leseni Tatu (03) ni za uchimbaji mdogo wa madini ujenzi na leseni Moja (01) ni ya uchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu.

Mheshimiwa Spika, GST ambayo ni taasisi yetu ya Jiolojia (Geological Survey of Tanzania) inaendelea kuhuisha kitabu chake cha madini yapatikanayo katika Mikoa yote Tanzania Bara na kwa sasa tayari Mkoa wa Tabora na Wilaya zake ikiwemo Wilaya ya Urambo ni moja kati ya mikoa itakayofanyiwa utafiti kwa lengo la kuhuisha kitabu hicho.

Mheshimiwa Spika, mara baada ya utafiti huo kukamilika, ramani ya uwepo wa madini hadi ngazi ya kijiji itaandaliwa na wananchi kupata taarifa hizo kupitia Serikali ya Kijiji na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya. Taarifa hizo zitawasaidia wananchi wote ikiwa ni pamoja na wananchi wa Wilaya ya Urambo kuwekeza katika sekta ya Madini kwa ujumla.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Minara katika maeneo yasiyo na minara na kutatua matatizo ya mawasiliano katika maeneo yenye Minara?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) inatekeleza miradi ya kufikisha huduma za mawasiliano katika kata tatu za Ugalla, Itundu na Vumilia Wilayani Urambo ambapo ujenzi wa minara unaendelea na utakamilika ifikapo Julai 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imepanga kufikisha huduma za mawasiliano ya simu Kata za Kiloleni, Kasisi, Itundu na Uyogo katika mwaka wa fedha wa 2022/ 2023 baada ya kubaini uwepo wa changamoto za mawasiliano katika baadhi ya maeneo ya vijiji katika kata hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata hizo zimejumuishwa katika zabuni inayotarajiwa kutangazwa kabla ya mwaka wa fedha wa 2021/2022 kukamilika kupitia Mradi wa Tanzania ya Kidijitali. Utekelezaji wa miradi hii ya usimikaji wa minara ya mawasiliano utahusisha uboreshaji wa mawasiliano ili kukidhi mahitaji ya upatikanaji wa huduma za intaneti katika Kata za Songambele na Imalamakoye asante.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, lini mpaka wa Hifadhi ya Ugalla utarekebishwa ili kurejesha kwa wananchi eneo walilokuwa wanatumia kwa ufugaji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Taifa Ugalla ilianzishwa kwa Sheria ya Hifadhi za Taifa, Sura 282 baada ya kupandisha hadhi Pori la Akiba Ugalla kwa Tangazo la Serikali, G.N. No. 936 la mwaka 2019.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa eneo hili ni muhimu kiuhifadhi na ndani yake kuna vyanzo vya maji, kabla ya kubadilishwa hadhi eneo hili lilihusisha shughuli za uvunaji zikiwemo ufugaji nyuki na uvuvi. Hali hii ilileta changamoto za kiuhifadhi ikiwemo uchomaji moto unaoathiri uoto wa asili na uchafuzi wa vyanzo vya maji. Hivyo, Serikali haioni haja ya kufanya marekebisho ya mpaka wa Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, ni lini majengo yataongezwa katika Chuo cha VETA Urambo ili kuongeza fani ambazo hazitolewi kwa sasa?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuongeza baadhi ya majengo yanayokosekana katika Chuo cha VETA cha Urambo ili kuimarisha uwezo na ufanisi wa kutoa mafunzo kwa wananchi wa Urambo yatakayowawezesha kupata ujuzi na kutekeleza shughuli zao za kiuchumi kwa weledi na viwango stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali kupitia Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imetenga fedha kiasi cha shilingi 880,719,315.39 kwa ajili ya kukiimarisha Chuo cha VETA cha Wilaya ya Urambo. Fedha hizi zitatumika katika ujenzi wa miundombinu ya jiko, bwalo la chakula, madarasa na majengo mawili ya karakana. Aidha, ujenzi wa majengo hayo umeanza mwezi Mei, 2023.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya mawasiliano ya simu katika maeneo ambayo orodha yake iliwasilishwa Wizarani – Urambo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetekeleza ujenzi wa minara kumi katika kata 10 ambazo ni kati ya kata 18 za Wilaya ya Urambo, ambapo minara tisa imekamilika katika Kata za Imalamakoye, Kasisi, Songambele, Itundu, Ukondamoyo, Nsenda, Uyogo, Vumilia, Ugalla pamoja na Uyumbu.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuboresha upatikanaji wa huduma ya mawasiliano katika baadhi ya Vijiji vya Kata ya Kasisi na Kiloleni na tayari imekwisha wapata watoa huduma wa kufikisha huduma ya mawasiliano katika kata hizo. Kwa upande wa kata za Kapilula, Kiyungi, Mchikichini na Muungano, Serikali kupitia UCSAF itafanya tathmini ili kupata hali halisi ya changamoto ya mawasiliano katika maeneo hayo.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Je, lini Serikali itaendeleza barabara ya Mpanda - Kahama ili ifike Ulyankulu - Urambo - Ussoke - Tutuo - Sikonge hadi Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANROADS inaendelea na kazi ya ujenzi wa barabara hizi kwa awamu kwa kiwango cha lami ambapo upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya kutoka Mpanda – Ugalla – Kaliua – Ulyankulu hadi Kahama urefu wa kilometa 457 umekamilika na sehemu ya barabara kutoka Urambo hadi Ussoke kilometa 45 tayari imejengwa kwa kiwango cha lami. Kwa sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara za Ulyankulu hadi Urambo na Tutuo hadi Ussoke na baada ya kukamilika kwa usanifu huo Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hizi kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-

Je, mafanikio gani yamepatikana kupitia mpango wa umeme jazilizi na lini Kituo cha kupooza umeme cha Uhuru kitafanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwaza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Tabora una jumla ya vitongoji 122 vilivyonufaika na mradi wa umeme jazilizi (densification) ambapo kati ya hivyo, vitongoji 27 vipo katika Jimbo la Urambo. Mradi huu wa umeme jazilizi unatarajia kuunganisha umeme katika majengo, makazi, na shule 7,209 ambapo kati ya hayo, 1,722 yapo katika Jimbo la Urambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Kupooza Umeme cha Uhuru kipo kwenye mradi wa kuunganisha umeme wa Gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kigoma ambapo katika mradi huo, njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Kidahwe Mkoani Kigoma itajengwa. Mradi huo utahusisha pia ujenzi wa vituo vitatu vya kupooza umeme msongo wa kilovoti 132 kuja 33 vya Urambo, Nguruka na Kidahwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mradi wa Kuimarisha Gridi ya Taifa (The National Grid Stabilization Projects) imetenga jumla ya Shilingi bilioni 24 katika mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya kujenga njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Urambo yenye urefu wa kilometa 115, na kukamilisha kituo cha kupooza umeme cha Urambo kilichoko Uhuru. Hivyo, kituo cha Kupooza Umeme cha Uhuru kitaanza kufanya kazi mwezi Juni, 2023 ambapo inatarajiwa kuwa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Tabora hadi Urambo itakuwa imekamilika, nashukuru.