Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Hussein Ali Mwinyi (9 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia hoja iliyo mbele yetu jioni ya leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita katika kujibu hoja zilizotolewa na Msemaji wa Kambi ya Upinzani juu ya role iliyochukuliwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kipindi cha uchaguzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msemaji wa Kambi ya Upinzani alianza kwa kusema kwamba Zanzibar imetekwa na Jeshi la Tanganyika tangu kipindi cha uchaguzi wa kwanza hadi wa pili na majeshi yako Zanzibar in full combat kana kwamba nchi iko katika vita. Naomba nimueleze Mheshimiwa Msemaji wa Kambi ya Upinzani kwamba hakuna Jeshi la Tanganyika. Nitawaomba Waheshimiwa Wabunge kwa kufuata Katiba ya nchi, jeshi ni moja na ni Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa maana ya kujibu swali la kuwa kwenye combat, naomba nimuelimishe Mheshimiwa kama ifuatavyo. Kazi kubwa tatu za Jeshi ni ulinzi wa mipaka, ulinzi wa amani na kutoa msaada kwa mamlaka za kiraia au vyombo vingine vya ulinzi na usalama wanapohitajika kufanya hivyo. Hili suala ni la Kimataifa wakati wa uchaguzi majeshi yote yanakuwa standby. Ndiyo maana jeshi linakuwa kwenye combat kwa sababu ni kipindi cha standby, cha tahadhari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawaishii kuwa standby tu hata major installations katika nchi zinalindwa na jeshi wakati wa uchaguzi. Bandari, viwanja vya ndege, redio na televisheni na sehemu ambazo ni za uzalishaji mkubwa wa umeme na kadhalika, wakati huo vinalindwa na jeshi kwa sababu ya kuweka tahadhari. Kwa hiyo, hiyo ndiyo sababu kwa nini walikuwa kwenye combat na hii ni ya Kimataifa unaweza uka-check nchi yoyote wakati wa uchaguzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili alilolizungumzia Mheshimiwa alisema Jeshi la Tanganyika linatumika kuulazimsha Muungano. Kama nilivyosema awali kwanza hakuna Jeshi la Tanganyika. (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Hata hivyo, niseme kwamba Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania ni kielelezo cha Muungano wenyewe. Toka tulipoungana mwaka 1964, jeshi limekuwa ni moja, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania pande zote mbili. Kwa hiyo, hakuna suala la kulazimisha utawala, ni suala la kwamba jeshi liko Zanzibar kwa madhumuni ya kulinda mipaka ya nchi yetu kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa alisema katika uchaguzi wa marudio, Serikali ya Muungano ilipeleka majeshi na silaha Zanzibar ili kuhakikisha kuwa malengo yao ya kuendelea kuitawala Zanzibar kimabavu yanaendelea.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Niwaeleze Waheshimiwa kwamba Jeshi toka mwaka1964 lina vikosi vyake Zanzibar. Vikosi hivyo kwa taarifa yenu si kwamba havina silaha siku zote silaha zipo. Tuna haja gani ya kupeleka wanajeshi, tuna haja gani ya kupeleka silaha wakati wa uchaguzi wakati miaka yote viko kule. Tunachosema jeshi liko kule kwa madhumuni ya kulinda mipaka yetu na kuleta amani si vinginevyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema JWTZ limepata heshima kubwa katika medani za Kimataifa kwa nidhamu na uhodari wake wa kulinda amani katika nchi nyingine lakini Serikali ya Jamhuri ya Muungano imekuwa ikilitumia jeshi hili vibaya kwa kulipeleka Zanzibar kwenda kusaidia kufanya ghilba…
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Ya uchaguzi na hivyo kujikuta kwamba linashiriki katika uvunjifu wa amani badala ya kuleta amani. Mimi ninachosema ni kwamba, kwanza namushukuru kwa kuelewa kwamba jeshi letu lina sifa ya Kimataifa ya ulinzi wa amani. Nchi zote duniani zinalisifia jeshi letu kwa sababu ya weledi na nidhamu. Narudia kusema liko pale Zanzibar kwa madhumuni ya kulinda amani, kulinda mipaka yetu na sovereignty ya nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa aliendelea kusema kwamba Jeshi la Wananchi wakati wa uchaguzi lilikuwa likifanya uandikishaji wa wapiga kura katika makambi yao nje na utaratibu wa uandikishaji wa wapiga kura. Mimi nasema Mheshimiwa tumwogope Mungu.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haijawahi kutokea na wala haitatokea watu kuandikishwa katika makambi ya jeshi.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Si kweli na kama unao ushahidi nitapenda niuone na hilo naweza nikakuhakikishia, jambo hili halipo kabisa. (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, aliendelea kusema kwamba Serikali ilieleze Bunge ni kwa nini inatumia vibaya Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika masuala ya kisiasa.
Mimi ndiyo nasema sasa kwamba nyie ndiyo mnaliingiza jeshi katika masuala ya siasa. Jeshi halijawahi kutumika kisiasa hata siku moja na mara zote nasema ni vyema Waheshimiwa Wabunge tukazungumza siasa zetu bila kuliingiza jeshi. Kwa sababu Jeshi la Wananchi wa Tanzania linafanya kazi nzuri ya kulinda amani na nakuambieni kukosa kuwa na Jeshi la Tanzania katika uchaguzi huu pale Zanzibar pasingekalika.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Si kweli na kama unao ushahidi nitapenda niuone na hilo naweza nikakuhakikishia, jambo hili halipo kabisa. (Makofi)
(Hapa baadhi ya Wabunge walikuwa wakiongea bila mpangilio)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, aliendelea kusema kwamba Serikali ilieleze Bunge ni kwa nini inatumia vibaya Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika masuala ya kisiasa.
Mimi ndiyo nasema sasa kwamba nyie ndiyo mnaliingiza jeshi katika masuala ya siasa. Jeshi halijawahi kutumika kisiasa hata siku moja na mara zote nasema ni vyema Waheshimiwa Wabunge tukazungumza siasa zetu bila kuliingiza jeshi. Kwa sababu Jeshi la Wananchi wa Tanzania linafanya kazi nzuri ya kulinda amani na nakuambieni kukosa kuwa na Jeshi la Tanzania katika uchaguzi huu pale Zanzibar pasingekalika.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuhitimisha hoja yangu jioni ya leo. Niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika hoja hii, wale waliochangia kwa kuzungumza ambao idadi yao ilikuwa ni 24 na wale waliochangia kwa maandishi ambao idadi yao ilikuwa ni 31. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Halima Mdee alinitahadharisha kwamba nisije nikasema muda wa kueleza umekwisha. Ukweli ni kwamba kwa idadi hii si rahisi kumgusa kila mmoja wenu. Nataka niwahakikishie kama kawaida yetu, baada ya kukamilisha kazi hii tutaleta majibu yote kwa maandishi kwa kila mchangiaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote. Leo asubuhi wakati tumeanza shughuli za bajeti hii ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa nilipata moyo sana kuona kwamba Wabunge wote wa pande zote mbili wakiwa wanaliunga mkono jeshi letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakubali kabisa kwamba, baada ya uchaguzi siasa huwa zinahamia Bungeni. Pia ni sahihi kabisa kila mmoja kupiga siasa humu ndani ya Bunge lakini naendelea kuwasihi Waheshimiwa Wabunge tujitahidi sana kutoliingiza jeshi katika siasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo kwa bahati mbaya sana, nadhani ni kwa sababu ya kuzidiwa tu na hisia zetu za kisiasa zimetoka kauli humu ambazo kwa kweli zisingepaswa kutoka lakini bado tunayo nafasi ya kujirekebisha. Naamini Waheshimiwa Wabunge wa Kambi ya Upinzani na wa Chama Tawala sote tunatambua mchango mkubwa wa jeshi katika nchi yetu na sote tunaliunga mkono na ndiyo maana asubuhi mlimshangilia sana Mkuu wa Majeshi kwa kutambua mchango wa jeshi katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kueleza maelezo hayo ya utangulizi, sasa naomba niingie katika hoja za Waheshimiwa Wabunge. Nitaanza na hoja za Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Kwanza walisema kwamba Serikali itoe fedha za maendeleo zitakazotengwa katika mwaka huu wa fedha kwa ukamilifu na kwa wakati na pia Serikali ilipe madeni yote yaliyohakikiwa na Hazina. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sote ambao ni Wabunge tunafahamu kwamba tunapanga bajeti lakini mwisho wa siku inategemea sana na makusanyo ya Serikali. Ni mategemeo ya kila mmoja wetu kwamba Serikali ikikusanya vyema kama ambavyo mwelekeo unaonesha, bila shaka fedha hizi zitapatikana na tutaweza kutekeleza yale ambayo tumeyapanga katika mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia imetakiwa tushiriki kubuni mbinu za kuzalisha mazao ya kiraia ili kuongeza mapato. Napenda kutoa taarifa kwamba mashirika yetu yote, Suma JKT, Mzinga na Nyumbu, yanafanya juhudi mbalimbali ya kuzalisha mali ili waweze kupata kipato cha ziada. Kwa mfano, shirika la Mzinga wanazalisha risasi za kiraia pamoja na milipuko kwa ajili ya migodi. Nyumbu wanazalisha power tillers na mashine za matofali. Suma JKT wanasindika mazao ya nafaka na uunganishaji wa matrekta. Aidha, mashirika haya yanaendeleza ubunifu mbalimbali ili kuweza kuongeza kipato chao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya wanajeshi zilengwe kwa askari wa vyeo vya chini. Hapa tunasema katika mradi huu unaoendelea sasa ambapo nyumba 6,064 idadi yote imeelekezwa kwa askari wa vyeo vya chini. Hivyo ushauri huu unaenda sambamba na mpango wetu. Ni awamu ya pili ambayo tunalenga kuwapatia nyumba maafisa na wale askari wa vyeo vya juu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi kumiliki maeneo ya ardhi kisheria. Suala hili tunalitambua ilikuwa ni kasoro kubwa. Siku za nyuma taasisi za Serikali zilikuwa zinapewa government allocation peke yake lakini kila siku zikienda na uhaba wa ardhi imekuwa kuna uvamizi katika maeneo haya na ndiyo maana sasa tumeona umuhimu wa kupima maeneo yote ya jeshi na kuyapatia hati ili waweze kumiliki kisheria. Wakati tunafanya hayo, tutaendelea kuhakikisha kwamba maeneo ya jeshi yanatunzwa hivyo kuweza kupunguza uvamizi unaotokea katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, upimaji na ulipaji fidia kwa maeneo ya jeshi ufanyike. Kama ilivyoelezwa kwenye hotuba yangu, ibara ya 60 na 61 katika ukurasa wa 43 na 44 na kufafanuliwa katika hoja Namba tatu ya ukurasa wa 57, Wizara itaendelea kushirikiana na mamlaka husika ili kukamilisha upimaji na ulipaji fidia kwa maeneo ya jeshi. Natambua Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia katika maeneo haya ya kutaka uthamini, upimaji na ulipaji wa fidia. Katika bajeti ya mwaka huu kama mtakavyoona katika fedha za maendeleo, tumeweka shilingi bilioni 27.7 lengo ni kuanza kupunguza yale maeneo ambayo yanahitaji kulipiwa fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi kutambua na kulinda mipaka yake. Jambo hili sasa linafanyika kwa nguvu zote, tunaweka mabango na tunapanda miti katika maeneo yetu ya mipaka ili wananchi waelewe fika wapi maeneo ya jeshi yanaanzia na wapi yanaishia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kurasimisha makabidhiano ya maeneo yanayotolewa na mamlaka za kiraia kwa jeshi na kuweka uzio maeneo yote ya jeshi. Ushauri umezingatiwa, tutashirikiana na mamlaka za mikoa kuhakikisha kumbukumbu za makabidhiano ya ardhi waliyoitoa kwa jeshi zinawekwa vizuri. Uwezekano wa kuweka uzio maeneo yote ya jeshi ni mdogo kwani maeneo hayo ni makubwa sana mfano eneo la Monduli, Tondoroni na Msata. Tunachoweza kufanya ni kuweka ukanda wa tahadhari yaani buffer zone na mabango ya tahadhari ya maeneo yote ya jeshi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la uboreshaji wa pensheni za wanajeshi wastaafu hasa kwa ngazi ya kuanzia Private hadi Brigedia Jenerali kwamba limefikia wapi. Serikali imetambua umuhimu wa kuboresha pensheni kwa wastaafu ikiwemo wanajeshi. Hivyo suala hili linaendelea kufanyiwa kazi kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Wizara ya Fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kutenga bajeti ya kutosha kuwezesha JKT kuchukua vijana wote wanaomaliza kidato cha sita kwa ajili ya mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria. Ushauri huu umepokelewa na ndiyo azma yetu. Hata hivyo, kama tulivyojibu, Wizara itaendelea kuwasiliana na Hazina ili kutoa fedha za kutosha kuliwezesha JKT kuchukua vijana wote wanaomaliza kidato cha sita kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria kwa wakati mmoja kadiri hali ya fedha itakavyoruhusu.
Mheshimiwa Naibu Spika, fidia kwa vijana wa JKT wanaoumia wakiwa mafunzoni. Wizara imepokea ushauri wa Kamati na itaufanyia kazi sanjari na kuboresha Sheria ya Ulinzi wa Taifa na sheria iliyoanzisha JKT.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maeneo hayo ambayo yalitolewa na Kamati ya Bunge ya Ulinzi na Usalama, naomba sasa niingie kwenye hoja ya Kambi ya Upinzani. Kwanza kulikuwa na hoja ya upendeleo katika ajira za jeshi. Labda nielezee kidogo utaratibu unaotumika katika ajira ili tuondokane na wasiwasi kwamba kuna upendeleo. Kwanza niseme tu kwamba ajira jeshini kwa sasa wanachukuliwa vijana ambao wako katika makambi ya JKT peke yake, jeshi halichukui tena uraiani. Kwa maana hiyo ni kwamba wale vijana wanaokwenda JKT wakati wa ajira wanafanyiwa usaili vijana hao, kwa hivyo sioni upendeleo unatokea wapi. Sasa hawa wa JKT wanapatikanaje? Kila mwaka tunatoa nafasi kupitia mikoa hadi wilaya, ili wilaya zenyewe zichuje vijana katika maeneo yao na kuwapeleka JKT. Kwa hiyo, hii hoja ya kwamba kuna upendeleo, kwa kweli sioni upendeleo huo utatokea wapi wakati hatuchukui uraiani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ilikuwa Wizara inalishughulikiaje suala la migogoro ndani ya vyama vya wanajeshi wastaafu. Jibu ni kwamba Wizara kupitia Makao Makuu ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, imevishawishi vyama vyote vya wanajeshi wastaafu kuunda chama kimoja tu cha Kitaifa ambacho kitaendeshwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za kijeshi. Hivi sasa kuna vyama kama alivyovitaja lakini viko chini ya kanuni za mashirika yasiyokuwa ya kiserikali (NGO‟s). Kwa hivyo, inatupa shida kama Serikali kufanya nao kazi na kuwasaidia kama inavyotakiwa lakini wakiwa chama kimoja ambao watafuata taratibu za kijeshi, bila shaka itakuwa rahisi kwetu kuwapa msaada utakaostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la uteuzi wa wanajeshi kwenye nafasi za kisiasa kama ilivyokwishasemwa na walionitangulia AG na wengine, ndugu zangu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inampa mamlaka Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumchagua mtu yeyote kwa nafasi yoyote. Kwa hivyo, haijavunjwa Katiba hapa na kwa utaratibu wa sasa wanajeshi wote hawaruhusiwi kujihusisha na vyama vya siasa. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu anayo mamlaka ya kumpangia kazi mwanajeshi yeyote kadiri anavyoona inafaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili napenda nikuambieni kwamba yapo maeneo ya nchi yetu ambayo yako katika mipaka yana changamoto nyingi za kiulinzi na usalama ndiyo maana ikaonekana ni busara kupeleka Wanajeshi. Kuna Wilaya kule kuna wakimbizi ambapo hali ya ulinzi na usalama imeharibika kwa sababu ya silaha zinazoingizwa, kwa sababu ya watu wanaoingia kwa mawimbi makubwa ya wakimbizi na kadhalika. Wakipelekwa wanajeshi kule experience imeonesha kwamba kazi ya ulinzi na usalama inafanyika vyema zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali iwaagize Wakuu wa Vikosi vyote vya JKT kutengeneza programu ya uzalishaji mali katika kilimo, uvuvi na mifugo. Kama ilivyoelezwa katika ibara ya 53 ya hotuba yangu, ushauri huu umepokelewa na taarifa za uzalishaji mali na mapato itaendelea kutolewa katika Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Ukweli ni kwamba programu za uzalishaji mali katika vikosi vyote vya JKT zipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itoe fedha zote zitakazotengwa katika bajeti ya Wizara ya Ulinzi. Hili ni kama nilivyosema awali, itategemea sana na mapato ya Serikali lakini ni mategemeo yetu kwamba kwa sasa kwa sababu ukusanyaji ni mzuri, hatuna shaka kwamba fedha zilizotengwa zitaweza kupatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niingie katika kile kisehemu ambacho kilikuwa kinazua mgogoro, nacho ni jeshi kuingilia kazi za polisi Zanzibar. Ndugu zangu nataka niseme, wakati nachangia hotuba ya Ofisi ya Makamu wa Rais nilitoa maelezo ya kina na nilidhani tumeelewana ni kwa nini jeshi wakati wa uchaguzi linakuwa standby. Narudia kusema kwamba wakati wa uchaguzi au nianze kwa kuelezea majukumu ya jeshi, majukumu ya jeshi makuu ni matatu. Kwanza ni ulinzi wa mipaka yetu; pili ni ulinzi wa amani; na tatu ni kutoa msaada kwa mamlaka za kiraia na vyombo vingine vya ulinzi na usalama wanapohitajika kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wakati wa uchaguzi Zanzibar, jeshi liliona ni muhimu kukamata major installations kwa ajili ya usalama. Maeneo ya airport, bandari, redio na maeneo mengine kama hayo vililindwa na jeshi kwa ajili ya kuhakikisha usalama wa ziada lakini hakukuwa na nia ya kumtisha yoyote, nia ilikuwa ni kuleta usalama. Kama walivyosema wengi hapa, naomba nirudie kauli ile kwamba, walinzi ni walinzi anayeogopa mlinzi ni mhalifu. Hakuna sababu kwa nini uwaogope walinzi kama huna nia mbaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunachosema ni kwamba, wanajeshi walikuwa on standby endapo itatokea vurugu na mamlaka ya vyombo vingine vya ulinzi na usalama watahitaji msaada wao wawe tayari kutoa msaada. Hata hivyo, ukweli unabaki pale pale kwamba wakati wa uchaguzi, ninyi ni mashahidi, mimi pia nilikuwa Zanzibar nimepiga kura, sehemu zote zilikuwa zinalindwa na polisi, jeshi walikuwa kwenye barracks zao isipokuwa hizo major installations nilizoelezea hapa, basi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja kwamba ni faida gani tunapata kwa JWTZ kushiriki katika operesheni za amani. Kwanza nishukuru kwa wote waliochangia na kusema kwamba kazi inayofanywa na jeshi kwenye ulinzi wa amani ni nzuri, tumepata sifa nyingi na tunawaunga mkono wanajeshi wetu waendelee kutuwakilisha vyema sehemu hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, faida tunazozipata kwanza tunapata uzoefu wa Kimataifa na mbinu mpya. Pili, wanajeshi binafsi wanafaidika kwani hupata kipato kwa kushiriki ulinzi wa amani. Tatu, ulinzi wa amani umeliletea sifa jeshi letu Kimataifa. Katika takwimu za ubora zilizotolewa hivi karibuni jeshi letu Kimataifa lipo katika nafasi ya 27 ndiyo sababu sisi tunapata nafasi nyingi za kwenda kulinda amani katika nchi mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee na hoja nyingine kama ifuatavyo:-
Ushauri wa kutumia vyombo katika shughuli za maendeleo na uzalishaji. Hili alilitoa Mheshimiwa Shamsi Nahodha nadhani nimeshalisema kwamba taasisi zetu zote zinafanya kazi hii ya kuzalisha mali na kufanya tafiti ili ziweze kupata kipato cha ziada.
Vijana wanaomaliza JKT wasiachwe bila ajira. Kama nilivyosema na alivyosema Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, tuna mambo mawili, si rahisi kuwaajiri vijana wote ambao wanaingia JKT, lakini ni lazima tujipongeze kwa sababu tumefanya kazi nzuri. Takwimu zinatuonesha kuanzia mwaka 2001 - 2015, kati ya vijana wote waliochukuliwa katika makambi ya JKT walioajiriwa ni asilimia 72.9, hawa wameingia katika vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama.
Mheshimiwa Naibu Spika,Waliobaki ambao ni wachache kama asilimia 30 sasa ndiyo tumekuja na mpango huu wa uwezeshaji, wanapewa mafunzo kule na wakitoka watapewa mitaji ili waweze kujiajiri wao wenyewe. Kusema kuwaajiri asilimia 100 haiwezekani, ingekuwa vyema na ningependa iwe hivyo lakini kwa bahati mbaya bado uwezo wetu haujafikia hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na ushauri wa kuwa na database ya vijana wa JKT. Database hiyo ipo kwa wale wanaoajiriwa na wale wanaorudi nyumbani kwa sababu nao ni jeshi la akiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ilikuwa ni kuimarisha vyuo vya ufundi stadi JKT ili vijana wapate stadi za kazi. Ushauri umepokelewa, Wizara inaendelea kuchukua hatua za kuimarisha vyuo vya ufundi stadi JKT kwa kuviwezesha kivifaa na wataalam kadiri bajeti inavyoruhusu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro wa ardhi Tondoroni, Makuburi na Ihumwa. Tondoroni mgogoro umekwisha kupitia Mahakama kesi namba 48 ya mwaka 2005 ambapo Serikali ilishinda. Hata hivyo, wahusika halali walikwishalipwa fidia kupitia Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro wa Makuburi Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni imeandaa mchoro wa mipango miji kwa kuzingatia marekebisho ya mpaka mpya wa kambi ambapo eneo la jeshi litazungukwa na viwanja vilivyopimwa. Tulichofanya pamoja na kwamba wananchi walivamia eneo la jeshi tumeweka mipaka mipya wao tukawatoa nje ya ile mipaka kuweza kuwa-accommodate ili wasilazimike kuondoka au kulipwa fidia. Kwa maana hiyo, tatizo hapa naliona limekaa vizuri lakini manispaa nayo imechukua jukumu la kuwapimia wananchi wale ili wawe na hati na isiwe tena ni eneo ambalo halijapimwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Kambi ya Ihumwa halina mgogoro. Tatizo lililopo ni la eneo dogo la nyongeza ambapo taratibu za kulipima na kulifanyia uthamini bado hazijakamilika. Kama nilivyosema tukipata fedha tutakamilisha taratibu hizo ili tuweze kulimiliki kihalali.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Zungu alitaka pensheni za vyombo vya ulinzi na usalama ziwe na taratibu zake maalum badala ya taratibu hizi za kawaida za utumishi wa umma. Hili ni wazo zuri, tunalipokea na ushauri huu utazingatiwa na tutawasiliana na wenzetu wa Hazina na Ofisi ya Rais, Utumishi ili tuangalie ni jinsi gani tunaweza kufanya lakini sote tunakubaliana na ninyi kwamba kuna baadhi ya wenzetu ambao walistaafu zamani pensheni zao haziridhishi, ni ndogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu misheni zetu tunapokwenda nje ya nchi, walitaka kujua fedha za misheni, hili nadhani nimeshalijibu na nitoe tu ufafanuzi wa ziada kwamba ziko fedha ambazo zinapatikana ukiacha zile ambazo wanalipwa wanajeshi wenyewe, sisi tunawalipa asilimia 80 ya zile zinazolipwa kutoka kule UN lakini jeshi pia linapata fedha kwa ajili ya kuwa na zana zake kule na pili matengenezo na tatu kuweza kupeleka zana mpya. Kwa hiyo, malipo ya fidia ya UN yanatolewa na fedha hizo zinalipia posho kwa wanajeshi, kugharamia ukarabati wa zana, kununua vifaa na zana mpya, kuandaa vikosi vipya kwenda kubadili vile vinavyorejea na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja ya kutaka kujua tofauti ya Chapter Six na Chapter Seven katika malipo. Malipo ya fidia ya UN hayatofautishi kama ni operation ya Chapter Six au ya Chapter Seven, yote yanafanana na ni sawa, ni chapters zinazotofautisha utendaji katika eneo la ulinzi na amani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wanajeshi wetu waliopoteza maisha au kuumia kwenye operations hizo wote walishalipwa kikamilifu kwa mujibu wa taratibu za UN na za JWTZ. Kwa sasa hakuna familia yoyote inayolidai jeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine lililochangiwa lilikuwa ni suala la Duty Free Shops kama alivyochangia Mheshimiwa Maryam Msabaha kwamba bidhaa zinazouzwa kule hazina nafuu na zile zinazouzwa mitaani. Tumepata malalamiko haya na nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili tunalifanyia kazi kwa nguvu kabisa. Lengo letu ni kwamba mashirika yetu ya jeshi ndiyo yaendeshe maduka haya ikiwemo Mzinga ambao wameshaanza katika baadhi ya vikosi, tunataka Suma JKT waingie ili hatimaye maduka yote ya jeshi yaendeshwe na jeshi lenyewe na kwa kufanya hivyo tutaondokana na tatizo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, huduma za mabwalo kweli tunalo tatizo na kazi ya ukarabati wa mabwalo linatekelezwa kwa kadiri bajeti zinapopatikana. Ni kweli kwamba mabwalo mengi kwa sasa hali yake sio nzuri kutokana na uhaba wa bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri kuhusu bajeti, madeni na maeneo ya jeshi, nadhani hili tumeshalitolea ufafanuzi. Tumesema kwamba bajeti ikiruhusu tutahakikisha tunaondoa matatizo yote haya yanayoonekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali moja lilikuja kuhusu wastaafu kulipwa kila mwezi. Tunachosema ni kwamba wala hatuna tatizo na wastaafu kulipwa kila mwezi kwa sababu hapo awali wastaafu walikuwa wanalipwa kila mwezi, ni wastaafu wao wenyewe waliomba kwamba sasa walipwe kwa miezi sita, walidai kwamba ile pensheni ya kila mwezi ni ndogo na wanakuwa wameshakopa, kwa hiyo, angalau wapewe ya miezi sita, wakapewa ya miezi sita. Baadaye wakabadilisha wakasema hiyo inakuwa muda mrefu sana, wakaletewa ya miezi mitatu. Kwa hiyo, kama sasa hivi wako tayari kurudi mwezi mmoja wala sioni tatizo lolote, haya ni matakwa ya wastaafu wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uanzishwaji wa bima ya afya kwa wanajeshi hili tunalipokea na tunaona umuhimu wake. Bima ya afya kwa wanajeshi ni muhimu kwa sababu sasa hivi tunapata shida sana, bajeti ya kutoa huduma za afya jeshini haitoshelezi na kwa maana hiyo tunao mpango wa kuanzisha bima kwa ajili ya wanajeshi wote, wawe kazini au wastaafu ili hatimaye tuondoe matatizo yao ya kupata huduma zinazostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo yaliyochangiwa kama nilivyosema ni mengi, naomba sasa niingie kwenye hoja za Mheshimiwa Sophia Mwakagenda. Anasema Amiri Jeshi Mkuu kuvaa sare za jeshi yeye anaona hili sio sawasawa. Kwanza nieleze kwamba Uamiri Jeshi Mkuu siyo cheo bali ni wadhifa. Kwa mujibu wa taratibu za kijeshi, Amiri Jeshi Mkuu anapoamua kuvaa sare ya jeshi katika shughuli yoyote ile ya kijeshi kama vile kufika katika eneo la mazoezi ya kijeshi, anaruhusiwa kwa mujibu wa taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili wala halijaanza hapa kwetu wala halijaanza katika awamu hii, Baba wa Taifa alivaa sare za jeshi, hapo nchini Kenya juzi juzi tu tumeona Rais Kenyatta kavaa sare za jeshi. Sioni kwa nini hii inakuwa hoja kubwa kwa sababu yeye ndiye Amiri Jeshi Mkuu. Anapoamua kuvaa afanane na wanajeshi wakati anaenda kwenye mazoezi yao wala hakuna tatizo hata kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wanajeshi wastaafu kuvaa sare za jeshi, maelezo ni kwamba mwanajeshi mstaafu anaweza kuvaa sare za jeshi katika shughuli yoyote lakini awe amepata kibali cha Mkuu wa Majeshi. Mkuu wa Majeshi huwa anatoa vibali hivyo kwa shughuli maalum ikiwemo ile ya kuapishwa Wakuu wa Mikoa alitoa kibali wavae kwa sababu wala hakuna tatizo, wale ni wanajeshi kwa sasa baada ya kustaafu ni jeshi la akiba, watakapohitajika wakati wowote wanaitwa ili waweze kufanya kazi za jeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kai alikuwa na hoja ya kukosekana kwa fedha za maendeleo kwa Ngome. Hili nimeshalizungumza toka awali, tunaelewa changamoto za bajeti na hii ni kwa Serikali nzima na wala siyo Wizara ya Ulinzi peke yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja pia kukosekana kwa fedha za kulipia fidia maeneo ya ardhi. Kama nilivyosema mwaka huu tumetenga shilingi bilioni 27.7, ni mategemeo yetu kwa kiwango kikubwa tutaweza kupunguza tatizo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, uchaguzi wa marudio Zanzibar. Jeshi kupelekwa Zanzibar Waziri atafute maneno mengine lakini siyo kwamba hawakupelekwa. Ndugu zangu naomba nirudie, nilisema hivi, watu wakisikia kwamba tunasema jeshi lilipelekwa Zanzibar wakati wa uchaguzi kila mtu atadhani jeshi halipo Zanzibar. Zanzibar kuna brigade siyo platoon wala siyo kombania kuna brigade. Brigade ya askari wa infantry iko Zanzibar na isitoshe kuna vitengo vya wanamaji, kuna vitengo vya airforce. Sasa tunapokuwa tunabishana kwamba jeshi lilipelekwa au halikupelekwa, naona haina msingi sana kwa sababu tayari jeshi lipo Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi liko Zanzibar kwa dhumuni moja tu, nalo ni kulinda mipaka ya nchi yetu ya ujumla ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndiyo kazi yake ya msingi kulinda mipaka yetu. Kwa hiyo, haiwezekani wasiwepo wakati mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iko mpaka kule Zanzibar. Kwa hiyo, nadhani kama walipelekwa au hawakupelekwa isiwe hoja, hoja ni kwamba jeshi liko pale kwa kazi moja ya kulinda mipaka yetu na wakati wa uchaguzi kama ilivyo international standard kwa nchi zote wanajeshi wanakuwa standby ili kukitokea machafuko waweze kusaidia, basi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi limetumika kuwatisha watu waliotulia. Mimi nasema jeshi limekuweko pale kusaidia watu watulie kwa sababu matukio yalikuwepo na wala hatuwezi kukataa. Mabomu yalirushwa wala sisemi mimi vyombo vya habari vimesema karibia na uchaguzi na wakati wa uchaguzi si kulikuwa na mabomu ya mkono yanarushwa, si yalitokea? Sasa kweli jeshi lisingekuwepo ile hali ya usalama na amani ingekuwepo mpaka leo? Sisi tunasema jeshi liko pale kwa kazi moja ya kulinda amani si kwa kazi ya kumtisha mtu yeyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja kwamba wanajeshi wa ngazi ya chini wanalipwa ration allowance tofauti na wa ngazi ya juu, si kweli. Jeshini ration allowance ni moja tu, anayopata private na anayopata general ni hiyo hiyo. Kama umepata taarifa kwa mtu yeyote si kweli, hapa nakataa kabisa, ration allowance ni hiyo hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Fakharia anasema nafasi za ajira za Zanzibar, kwa nini vijana wasichukuliwe kutoka JKU badala ya kupitia mikoani na wilayani. Jibu ni rahisi, sisi huwa tunapeleka nafasi za Zanzibar kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Tunawaachia uhuru wa kuamua wanazigawa kwa taratibu gani. Wakiamua kupeleka mkoani na wilayani ni juu yao, wakiamua kupeleka JKU ni juu yao. Kwa hiyo, kama tunaona JKU ni utaratibu mzuri zaidi kwa pamoja sisi Wabunge wa Zanzibar tuishauri SMZ ichukue vijana hao kupitia JKU. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nyumba za makazi zijengwe na Unguja pia, hii iko katika mpango wetu wa Awamu wa II. Awamu ya I kwa Zanzibar ilianza Pemba na Awamu ya II tutapeleka Unguja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wanajeshi wastaafu kulazimika kwenda Bara kushughulikia mafao yao. Hili nalikubali kwamba ni usumbufu, hawa watu hawana fedha, wanatakiwa wasafiri mpaka makao makuu, tutatengeneza utaratibu ili brigade pale ishughulike na mafao haya kwa kuwasaidia kuchukua maelezo yao wao wayapeleke makao makuu ili waweze kupata huduma kwa urahisi bila kusafiri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maswali ya Khadija Hassan Aboud ambapo yeye alishauri vijana wa JKT waajiriwe jeshini. Napenda kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba ndivyo tunavyofanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, aliendelea kushauri JKT iwe na aina mbili za mafunzo wale wa ujasiriamali na wale wa kuingia jeshini, tunadhani kwa sasa huo hautakuwa utaratibu mzuri sana kwa sababu uwezo wa kufanya hivyo hatuna. Hata hivyo, ikumbukwe kwamba lengo la JKT si kutoa ajira ni kuwafunza vijana wetu wa Kitanzania uzalendo, utaifa na kuhakikisha kwamba wakiwa pale basi wanapata mafunzo ya kijeshi lakini pia ujasiriamali kwa maana ya stadi za kazi ili waweze kujiajiri. Kwa hiyo, hili tutalitazama kwa wakati ujao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niingie katika hoja za Mheshimiwa Kubenea ambazo kwa kweli zimenisikitisha sana kwa sababu hazina punje ya ukweli ndani yake. Nasikitika kusema kwamba Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano anaweza akachukua maneno ya mitaani akaingia nayo ndani ya Bunge akayasema bila ya kuwa na ushahidi, hii ni hatari tena ni hatari kubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwarifu Mheshimiwa Kubenea, sijui kama yupo humu ndani…
(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walikuwa wakiongea bila mpangilio)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, tuhuma anayoitoa kwamba jeshi limeingia mkataba na kampuni inayoitwa Hainan Construction ambapo jeshi litatoa eneo kubwa la ardhi kwa kampuni hiyo ili ijenge nyumba na kwamba kampuni hiyo itatumia kwa miaka 40 hazina punje ya ukweli ndani yake. Si kweli na naku-challenge ukiweza kuniletea uthibitisho huo mimi nitajiuzulu kwa sababu maneno unayoyasema ni ya mitaani. Nasikitika sana Mheshimiwa Mbunge kuleta maneno yasiyokuwa na uthibitisho kwa sababu maneno hayo ni ya uwongo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili alilolisema ambalo limenihuzunisha zaidi, anasema kampuni hiyo hiyo itaingia mkataba pia wa kumjengea nyumba Dkt. Hussein Mwinyi, huu siyo mgongano wa kimaslahi? Naliomba Bunge lako litumie utaratibu wa kikanuni, Mheshimiwa Kubenea akishindwa kuthibitisha maneno haya achukuliwe hatua stahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kwa sababu tusije ndani ya Bunge tukaharibu majina ya watu, tukawadhalilisha kwa sababu tu ya kuwa na uhuru wa kuzungumza ndani ya Bunge na immunity tunayopewa. Nasema uhuru tunao, immunity tunayo lakini kudhalilisha watu kwa maneno ambayo hayana ushahidi kukomeshwe. Huu ni uwongo mtupu, hakuna jambo kama hili. Kwanza hiyo kampuni hata kuwajua siwajui. Pili, haiwezekani maneno haya akayaleta kama hakuna mkataba wa ushahidi kama anao alete tuuone, hakuna hiki kitu, ni uwongo mtupu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kubenea aliendelea kusema kuwa kuna tuhuma za udhalilishaji kwa wanajeshi wetu waliokwenda kulinda amani Kongo, je, ni hatua zipi zimeshachukuliwa hadi hivi sasa? Nataka nimweleze Mheshimiwa Kubenea kwamba, tuhuma zinapotolewa ni wajibu wa mamlaka zinazohusika kuchunguza, huwezi kuvamia tuhuma ukachukua uamuzi. Jeshi liliunda Bodi ya Uchunguzi, wamekwenda Kongo kwa kushirikiana na Umoja wa Mataifa ufanyike uchunguzi wa kina ili watakapokuja kutoa taarifa za uchunguzi na ikithibitika kwamba kuna unyanyasaji wa kijinsia ulifanyika au walifanya askari wetu hatua za kinidhamu zitachukuliwa dhidi ya waliofanya vitendo hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi hili linaendeshwa kwa mujibu wa sheria na kanuni za jeshi, kwa hivyo, hakuna mtu anayeruhusiwa kufanya jambo lolote kinyume na utaratibu akaachiwa lakini tunachosema uchunguzi ni lazima ufanyike. Udhalilishaji uliosemwa na Umoja wa Mataifa ni pamoja na ubakaji, baadhi ya watu wamedai katika ubakaji huo wamepata watoto, unafanyaje uamuzi wa kwamba huyu amekosa bila kufanya DNA test ya kugundua kama hao watoto kweli ni wa huyo anayeambiwa ni baba yao? Kwa hiyo ni kwamba uchunguzi unaendelea na ni mategemeo yetu kwamba utakapokamilia na ukithibitika hatua stahiki zitachukuliwa. Hii ni kawaida kabisa wala Mheshimiwa asipate tatizo lolote hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja nyingine nyingi ambazo zimetolewa, lakini nadhani kwa ujumla wake nimezi-summarize kwa pamoja ili tuweze kupata maelezo ya ujumla lakini nitakuwa tayari kutoa maelezo ya ziada nitakapohitajika. Kama nilivyosema awali wakati wa vifungu pia nitakuwa tayari kutoa maelezo kwa kadiri yatakavyohitajika.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu jioni ya leo ili niweze kuhitimisha hoja yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika hoja hii na michango ilikuwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, waliochangia kwa maandishi ni Waheshimiwa Wabunge 38 na waliochangia kwa kuzungumza ni Waheshimiwa Wabunge 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee naomba niishukuru kwa dhati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama chini ya uongozi thabiti wa Mheshimiwa Balozi Adadi Rajabu kwa ushirikiano wao mkubwa katika kutekeleza mambo ya kikanuni kama ilivyoainishwa katika kanuni za Bunge, Toleo la Januari, 2016 kupitia masuala yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza walitembelea miradi ya maendeleo chini ya Wizara yangu; pili, walifanya tathmini ya utekelezaji wa mipango ya bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, walifanya uchambuzi wa makadirio kwa mwaka wa fedha 2016/2017; na mwisho, walitoa maoni na ushauri wa Kamati ambayo yalitolewa kwa kuzingatia uchambuzi wa mambo yaliyozingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Kamati katika maoni yake kuhusu miradi ya maendeleo kutopatiwa fedha kadri ya makadirio na hili limekuwa ni changamoto kubwa kwetu. Tunaendelea kuwasiliana na Wizara ya Fedha na Mipango ili kuona kwamba miradi hiyo inapatiwa kipaumbele kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha 2016/2017. Tatizo kubwa kwa muda mrefu limekuwa ni ufinyu wa makusanyo na kipaumbele kwa matumizi ya Serikali na vipaumbele mbalimbali vinavyoikabili nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama ilivyo ada, naomba nianze kujibu baadhi ya hoja ambazo zimetolewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kwamba Serikali iyapatie mafungu ya Ngome JKT na Wizara, fedha zote za maendeleo kwa mwaka wa 2016/2017. Kulingana na upatikanaji wa fedha zinazotokana hasa na mapato ya ndani, Serikali imekuwa ikitoa fedha za maendeleo kwa Wizara ili kuweza kutekeleza shughuli za maendeleo. Mfano, hadi kufikia mwezi Machi, 2017 Wizara ilikuwa imepokea jumla ya shilingi 35.9 bilioni sawa na asilimia
14.5 ya bajeti ya maendeleo. Kumekuwa na mawasiliano kati ya Wizara yangu na Hazina kuhusu Wizara kupatiwa fedha za maendeleo zilizobakia ili kukamilisha utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni Serikali itoe shilingi bilioni 27 zilizotengwa mwaka 2016/2017 kwa ajili ya kulipia maeneo yaliyochukuliwa na Jeshi kabla ya terehe 30 Juni, 2017. Katika mwaka wa fedha 2016/2017, Wizara ilitenga shilingi bilioni 27.7 kwa ajili ya kupima na kuwalipa fidia wananchi ambao maeneo yao yalitwaliwa kwa matumizi ya Jeshi. Hata hivyo, fedha hizi bado hazijatolewa hadi kufikia mwezi Machi, 2017. Wizara imekuwa ikiwasiliana na hazina kuhusu kupatiwa fedha kwa ajili ya kutekeleza shughuli za maendeleo ikiwemo fedha kwa ajili ya fidia za ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadaye nitatolea maelezo yale maeneo yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyazungumza kwa uchungu kabisa kuhusu fidia kwa maeneo yaliyochukuliwa na Jeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ni kwamba Serikali ipime ardhi inayomilikiwa na Jeshi na kuimilikisha kwa Jeshi Kisheria. Kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Na. 4 ya mwaka 1999 na Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 ya mwaka 1999, hakuna kipengele cha utoaji wa hatimiliki kwa Taasisi za Serikali likiwemo Jeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, mazungumzo yanaendelea kati ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa na Mamlaka husika ili hatimaye maeneo yote ya Jeshi yapewe hatimiliki bada ya kuzifanyia marekebisho Sheria hizo. Serikali kupitia Wizara husika na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, inaendelea na taratibu za kuibadilisha Sheria ya Ardhi Na. 4 na 5 ya mwaka 1999 ili kuziwezesha Taasisi za Umma likiwemo Jeshi kumilikishwa maeneo kwa hatimiliki ili kuondokana na utaratibu wa sasa wa kusajiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la Sera na Sheria ya Ulinzi; Kamati ilitaka Serikali ikamilishe mchakato wa kufanya marekebisho katika Sheria ya Jeshi la kujenga Taifa, Sura ya 193 na Sheria ya Ulinzi wa Taifa, Sura ya192 ili iweze kuendana na wakati, mifumo ya utawala na mahitaji ya sasa ya Kisheria katika Sekta ya Ulinzi.

Mheshimiwa mwenyekiti, kwa kuwa suala la Sera ya Ulinzi wa Taifa ni la Muungano, kukamilika kwake kunategemea ridhaa ya pande zote mbili za Muungano. Hatua iliyofikiwa kwa sasa ni kupata maoni kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, marekebisho ya Sheria ya Ulinzi wa Taifa na Sheria ya JKT yatafanyika baada ya kukamilika kwa Sera ya Ulinzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, napenda nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba tumefikia sehemu nzuri sana, nimefanya mazungumzo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais anayeshughulika na vikosi vya SMZ kule Zanzibar na ameniahidi kwamba sera hii sasa inakaribia kupata maoni ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ili tuweze kukamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni Serikali ione muhimu wa suala la fidia kwa vijana wanaopata ulemavu wakiwa katika mafunzo ya JKT. Napenda kuliarifu Bunge lako kwamba malipo ya fidia hufanyika kwa mujibu wa Sheria ya Ulinzi wa Taifa ya mwaka 1966 ambapo mapendekezo ya marekebisho ya Sheria tajwa yatafanyika baada ya kukamilika kwa Sera ya Ulinzi wa Taifa. Kwa sasa, kijana analipwa fidia kwa kutumia kiwango cha mshahara wa Askari wa cheo cha Private kwa mwaka wa kwanza. Maana yake ni kwamba vijana wanaokwenda JKT wakiumia, siyo kwamba hawalipwi fidia, wanalipwa fidia kwa kutumia kigezo hiki cha kwamba tunawalipa sawa na aliyeajiriwa katika ngazi ya Private anapokuwa ni mwaka wake wa kwanza Jeshini. Kwa hiyo, fedha hizi huwa wanazipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni Serikali itoe kipaumbele kwa vijana waliopitia mafunzo ya JKT wakati wa kuajiri vijana kwa ajili ya shughuli za ulinzi katika Shirika la SUMA JKT. Hivi ndivyo hasa ilivyo. Napenda kutoa taarifa kwamba SUMA JKT Guard Limited linatoa kipaumbele kwa vijana waliopitia mafunzo ya JKT wakati wa kufanya ajira zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni Serikali iboreshe miundombinu ya kambi za JKT ili vijana wengi kwa mujibu wa Sheria waweze kufanya mafunzo hayo na kutenga fedha kwa ajili ya shughuli za uendeshaji wa mafunzo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inaendelea kuwasiliana na Mamlaka husika ili kuona uwezekano wa kuongeza fedha kwa mafunzo hayo kadri hali ya kifedha itakavyoruhusu. Sisi sote tunapenda kwamba vijana wote wanaokamilisha masomo yao ya kidato cha sita waweze kuingia Jeshini kwa mujibu wa sheria kabla hawajaendelea na elimu ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu eneo la madeni, Kamati imeitaka Serikali ilipe madeni ya Wazabuni na madeni ya Kimkataba. Serikali ione umuhimu wa kuongeza kasi ya kulipa madeni yote ya Wizara yaliyohakikiwa kiasi cha shilingi bilioni 212.3. Maelezo ni kwamba kiini cha madeni ya Jeshi ni ufinyu wa bajeti katika maeneo mbalimbali ya utekelezaji wa majukumu ya kijeshi. Jumla ya madeni yaliyohakikiwa na ambayo yanapaswa kulipwa ni shilingi bilioni 95.6. Mpaka sasa Serikali imechukua hatua ya kuanza kulipa madeni hayo ambapo imetoa shilingi bilioni 5.16. Aidha, madeni ambayo hayajalipwa ni shilingi bilioni 90.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara katika mwaka wa fedha 2016/2017, imelipa shilingi milioni 61.2 kwa ajili ya malipo ya Wazabuni wa ndani ambao wametoa huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa upande wa Wazabuni wa nje Wizara imelipa shilingi bilioni 30. Aidha, Wizara inadaiwa deni la kimkataba, mikataba mbalimbali kiasi cha shilingi bilioni 785.2. Kwa hiyo, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Wizara imekasimia shilingi bilioni 120.7 kwa ajili ya kulipa madeni ya kimkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fungu 39 la JKT jumla ya madeni ya fungu hili hadi kufikia mwezi Aprili, 2017 ni shilingi bilioni 101 na madeni yaliyohakikiwa ni shilingi bilioni 79.8. Serikali imeweza kulipa shilingi bilioni 4.2, hivyo kufanya deni hilo lililohakikiwa kubaki shilingi bilioni 75.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kuhusu SUMA Guard ilipwe madeni yake na wale ambao wamepewa huduma naye. Tumepokea ushauri wa Kamati kuhusiana na Kampuni ya SUMA JKT Guard Limited, kampuni itaendelea kufuatilia madeni kwa washitiri wake kwa kutumia Wakala wa kukusanya madeni na kuimarisha kitengo chake cha ukusanyaji madeni kwa ajili ya kufuatilia na kuwakumbusha wateja wake kulipa madeni yao.

Mheshimiwa Mwenyeki, kuhusu Mashirika ya Jeshi; Kamati imetaka Shirika la Mzinga kumilikiwa kisheria na kuwajibika chini ya mamlaka moja. Shirika la Mzinga ni Taasisi iliyo chini ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, lakini kama taasisi nyingine za Serikali au za Umma, linawajibika kuwa kwa Msajili wa Hazina vile vile. Wizara itashughulikia ushauri uliotolewa ili Shirika hili liweze kuwajibika chini ya mamlaka moja kwa kuanza utaratibu wa kubadilisha sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali itenge fedha za kutosha kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa miundombinu ili kuongeza ufanisi wa utendaji wa Mashirika ya Nyumbu na Mzinga; Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018 imetenga shilingi bilioni 8.8 kwa ajili ya kufanya ukarabati wa miundombinu ya teknolojia ya Shirika la Nyumbu na shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya Shirika la Mzinga. Hata hivyo, mashirika haya yataendeleza juhudi za mashirika yenyewe binafsi ili waweze kuzalisha fedha zaidi ambazo zitawasaidia katika kuboresha hali ya miundombinu ya mashirika haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ilikuwa ni sehemu ya kujibu hoja zilizotolewa na Kamati na sasa naomba niingie katika hoja zilizotolewa na Kambi ya Upinzani. Kabla sijaingia kwenye hoja zenyewe naomba niseme maneno machache ya utangulizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi ni Taasisi ambayo ni tofauti sana na taasisi nyingine za kiraia hasa kutokana na majukumu yake. Kila Mwanajeshi anapoingia Jeshini anafunzwa miiko na taratibu zake ambapo kwa sehemu kubwa ni kumwezesha Mwanajeshi kutumika vyema wakati anapohitajika kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika kwamba sehemu kubwa ya hotuba ya Kiongozi wa Upinzani au Msemaji wa Upinzani, imetokana na hisia na baadhi ya matamshi ambayo hayana ukweli wowote au hayajafanyiwa utafiti na matokeo yake yanaweza kuzua majungu au utovu wa nidhamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kwamba Jeshi huendeshwa kwa kuzingatia mambo yafuatayo:-

(1) Katiba ya Nchi;

(2) Sheria ya Ulinzi wa Taifa;

(3) Kanuni ya Majeshi ya Ulinzi; na

(iv) ni Forces Routine Orders zinazotolewa na Mkuu wa Majeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rejea zote zilizotajwa hapo juu, zinatoa utaratibu kamili wa namna ya kuendesha Jeshi kama Taasisi ya Nidhamu na Utii chini ya uongozi wa Amiri Jeshi Mkuu na pia uongozi wa Kisiasa wa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa katika uhalisia wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Ulinzi wa Taifa na Kanuni za Majeshi ya Ulinzi, volume ya kwanza, ya pili na ya tatu, zinatoa maelekezo ya namna Wanajeshi watakavyotenda kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani inaingilia mno shughuli za uendeshaji wa jeshi. Hatari iliyopo ni kwamba Kiongozi wa Upinzani amechukua maneno kutoka kwa Askari wasiozingatia nidhamu na bila ya kufanya utafiti wa kutosha, amegeuza kuwa ndiyo taarifa yake. Ni vyema tutambue kwamba kauli kama hizi zinaweza kupelekea kuligawa jeshi bila sababu yoyote au kupandikiza mbegu za utovu wa nidhamu jeshini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanajeshi wamejiunga na jeshi kwa masharti yaliyopo na wanapaswa kuyazingatia wakati wote wa utumishi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia kusema, nimesikitishwa sana na maneno yenye lengo la kuwagombanisha wanajeshi na Serikali yao pamoja na Wanajeshi na Uongozi wao wa juu. Hili halipaswi kuvumiliwa na ni vyema Bunge lako liangalie utaratibu wa kikanuni za kumtaka Msemaji athibitishe maelezo aliyoyatoa katika wakati muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo ya utangulizi, sasa naomba nizijibu hoja zilizotolewa na Msemaji wa Kambi ya Upinzani kama ifuatavyo:-

Kwanza, kuongeza muda wa kufanya kazi Jeshini baada ya muda wa kawaida kwisha. Siyo sahihi kuwa Wanajeshi hawakupewa au hawakuelezwa sababu za kuendelea kufanya kazi baada ya muda wa kazi za kawaida. Wanajeshi wote walipewa taarifa na hakuna taharuki yoyote. Muda wa kazi uliongezwa kwa ajili ya michezo na mazoezi ya viungo. Aidha, ikumbukwe kuwa wanajeshi wanaandikishwa kwa masharti ya kufanya kazi masaa 24. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la usalama wao; wanajeshi wanasafirishwa kwenda na kurudi kazini kwa kutumia mabasi maalum ya usafiri. Hapa nataka kusema kwamba, baada ya saa za kazi, ili Wanajeshi hawa wawe na utimamu wa kimwili na kiafya, wanatakiwa wafanye mazoezi ya viungo na hasa wajihusishe na michezo. Ndiyo sababu ya kuongeza muda wa kutoka kazini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani, ama kuna wakati pengine ilizoeleka kwamba watu wanamaliza baada ya muda wa saa za kazi wanakwenda bar wanakunywa pombe na kadhalika. Hii haina afya kwa jeshi letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi wanapokuja kurudisha taratibu stahili hatupaswi sisi kama viongozi kuwaona wanafanya makosa, badala yake tuwapongeze kwa hatua hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilikuwa ni kusitisha utoaji wa fedha za likizo kwa wanajeshi. Malipo ya fedha za likizo kwa wanajeshi hayajasitishwa na ni haki kwa wanajeshi wote. Aidha, siyo kweli kwamba Mnadhimu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, yaani Chief of Staff amezuia madai ya wanajeshi ya kulipwa malipo ya likizo. Mnadhimu Mkuu wa Jeshi amekuwa mstari wa mbele katika kufuatilia stahiki hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi kila mwaka wa fedha, fedha za likizo zinatengwa kutoka bajeti ya Jeshi kila mwaka wa fedha. Changamoto kubwa imekuwa ni ukomo wa bajeti, hali inayosababisha kutokidhi kuwalipa wanajeshi wote wanaostahili kwenda likizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara itaendelea kuwasiliana na Hazina iweze kusaidia kuongeza bajeti katika eneo hili ili wanajeshi wote waweze kwenda likizo. Aidha, Wizara inajaribu kubuni njia nyingine kwa kushirikiana na Hazina ili kuhakikisha kuwa wanajeshi wote wanalipwa fedha za likizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuongezea katika eneo hili; mimi binafsi wakati nikifanya ziara zangu katika Kambi za Jeshi, napata nafasi ya kuzungumza na Wanajeshi; katika kero kubwa ambayo imekuwa ikizungumzwa na Wanajeshi, ni kero ya fedha za likizo. Nimekuwa nikiwaambia kwamba hakuna mtu, siyo Wizarani wala Jeshini ambaye angependa wasipate. Sote tunapenda wapate, tunawapigania sana na tukifanikiwa katika kupata fedha hizi tutawalipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wote ambao hawajalipwa kwa kipindi ambacho walistahili, zinahesabiwa kama ni madeni. Fedha za madeni zikilipwa, watapewa fedha zao. Kwa hiyo, hatuoni sababu kwa nini kuja na dhana kwamba Chief of Staff anataka watu wasilipwe? Hili litahitaji kuthibitishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine iliyotolewa kwamba Wajumbe wa Bodi ya Manunuzi wanajipa safari za ununuzi wa zana nje ya nchi. Bodi ya Wazabuni ya JWTZ imeundwa kisheria kwa kuzingatia Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2011 na Kanuni zake. Bodi hiyo ina wajibu wa kutoa idhini ya manunuzi ya vifaa mbalimbali kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajumbe wa Bodi hiyo hawana wajibu wa kununua vifaa na hakuna Mjumbe wa Bodi ya Manunuzi ambaye amesafiri kwenda nje ya nchi kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya JWTZ. Utaona kwamba hoja hii nayo inataka ithibitishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani mtu mmoja barabarani akasema maneno ambayo kwa kweli yanaharibu taswira ya Jeshi zima, halafu tukayachukua tukayaweka kwenye hotuba halafu wengine tukanyamaza kimya. Kwa kweli hili litakuwa siyo jambo la busara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilikuwa ni kuondolewa kwa maduka ya bei nafuu Jeshini, yaani Military Duty Free Shops. Maduka hayo yaliondolewa rasmi na Serikali tarehe 1 Julai, 2016 baada ya kuonekana kutowanufaisha Wanajeshi na pia baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu kutumia mwanya wa maduka hayo kukwepa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuondoa maduka hayo, Serikali imekuwa ikiwalipa Wanajeshi fedha za ruzuku kama sehemu ya kupunguza makali ya misamaha ya kodi iliyoondolewa. Siyo kweli kwamba fedha hizo zimetolewa mara moja tu, fedha hizo bado zimeendelea kutolewa kila baada ya miezi mitatu kama Serikali ilivyoahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika, katika ziara zangu katika makambi ya Jeshi, ukiuliza matatizo ya Wanajeshi, wao wenyewe watakiri kwamba maduka haya yalikuwa yanawanufaisha wafanyabiashara siyo wao. Maduka mengi ya Jeshi, ilikuwa gharama wanazolipa wao ni sawa na kununua mtaani, wakati wao wametolewa ushuru. Kwa hiyo, aliyekuwa anafaidika ni wale wafanyabiashara. Serikali imegundua hili, sasa hivi wanatakiwa kulipwa; wameanza fitina na hili linaonekana kama vile Wanajeshi wanaonewa. Siyo kweli, waliokuwa wananufaika siyo Wanajeshi na tutaendelea kuwapa hiyo ruzuku ili kuweza kuwapunguzia makali ya maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tano, kuhusu Wanajeshi kutopandishwa vyeo. Suala la Wanajeshi kupandishwa vyeo, linazingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo bila ubaguzi wowote. Maafisa na Askari ambao wanastahili na wamekidhi vigezo, wamekuwa wakipandishwa vyeo mara kwa mara kwa kufuata taratibu zilizopo. Mara ya mwisho Maafisa na Askari wamepandishwa vyeo katika ngazi mbalimbali mwezi Aprili, 2017. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini? Maana yake, katika Hotuba ya Kambi ya Upinzani walitaka kuashiria kwamba, kuna Mkuu wa Majeshi mpya ameacha kupandisha watu vyeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepandisha watu vyeo. Kwanza kwa taarifa yenu, upandishwaji wa vyeo unafanywa na Kamati ya Ulinzi ya Taifa, ambayo Mwenyekiti wake ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Aprili mwezi uliopita tumekaa na tumepandisha vyeo Wanajeshi wote wanaostahili kupandishwa vyeo. Kwa hiyo, siyo kweli hata kidogo kwenda mitaani kuchukua maneno ambayo hayana chembe ya ukweli kuyaleta na kuyazungumza ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo ya fedha za chakula kwa Wanajeshi (Ration Allowance); fedha za chakula kwa Wanajeshi hulipwa kwa kuzingatia Sheria ya Ulinzi ya Taifa ya mwaka 1966; na Kanuni za Majeshi ya Ulinzi, Utawala ambapo chakula hutolewa kwa Wanajeshi kwa kuzingatia majukumu anayopewa Mwanajeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwanajeshi anawajibika kula chakula stahiki na mahali stahiki kwa mujibu wa kanuni na taratibu zilizopo. JWTZ kwa kushirikiana na Serikali, litaendelea kuhakikisha kuwa Wanajeshi wanapewa chakula stahili kwa kuzingatia majukumu wanayopewa. Fedha za chakula anazolipwa Mwanajeshi, siyo kwa ajili ya familia yake bali ni kwa ajili yake mwenyewe ili awe na afya imara, isiyotetereka ili aweze kutekeleza majukumu ya ulinzi wa Taifa kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niongezee kusema kwamba, wale ambao wapo kazini, wale ambao wapo kambini, wale ambao wana kazi maalum (operation), lazima wale ndiyo wakatekeleze operations. Wale ambao wapo katika maeneo mengine, wanapewa fedha zao kwenye
mishahara yao. Hakuna tatizo hapa. Kwa hiyo, haya maneno pia hayana ukweli Mheshimiwa. Naomba sana siku nyingine ukipata maelezo kama haya, nione kwanza, nitakupa taarifa kabla hujaweka kwenye hotuba yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine inahusu ufinyu wa bajeti ya umeme. Suala la ufinyu wa bajeti ya umeme, linatokana na ukomo wa bajeti unayotolewa na Serikali. Tunapenda kuishukuru Serikali kwa hatua iliyochukua ya kuweza kupunguza madeni ya umeme ili JWTZ liendelee kupata huduma ya umeme katika makambi. Wizara itaendelea kuwasiliana na Hazina ili waweze kutoa fedha za kutosha, katika eneo la umeme na maeneo mengine muhimu ambayo tunadaiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kweli kwamba Jeshi halilipi kwa kutotaka, wala siyo kweli kwamba Amiri Jeshi Mkuu ameamua hata Kambi za Jeshi zikatiwe umeme. Alichosema ni kwamba watu lazima walipe na baada ya hapo Hazina walitoa fedha na jeshi likalipa; na tutaendelea kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee na eneo lingine la utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2016/2017. Kambi ya Upinzani wanasema fedha za maendeleo zimetolewa pungufu, hili tunakiri. Fedha za Maendeleo hutolewa kila mwezi kutegemeana na mapato ya Serikali kila mwezi, Wizara inaendelea kuwasiliana na Wizara ya Fedha na Mipango ili fedha zote ambazo hazijatolewa, ziweze kutolewa katika kipindi kilichobaki ili tuweze kutimiza majukumu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu makusanyo kidogo ya maduhuli ya JKT; maduhuli ya JKT yaani Fungu 39 yanatokana na matunzo ya mazao ya shamba darasa, uuzaji wa nyaraka za zabuni na siyo kutoka katika shughuli za uzalishaji mali za SUMA JKT. Yaani kwa maana nyingine tutofautishe kati ya SUMA JKT na Fungu 39, yaani Makao Makuu ya JKT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii taarifa ya asilimia 31.8 ni maduhuli ya JKT, yaani Fungu 39 hadi kufikia Machi 2017. Aidha, hadi kufikia tarehe 15 Mei, 2017 fedha zilizokusanywa kutokana na maduhuli zimefikia asilimia 67.5 ya lengo. Kwa hiyo, tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika randama ya Fungu 57 subvote 1005 na subvote 2004 hazikutengewa fedha za mishahara. Je, vitengo hivi havina watendaji? Lilikuwa ni swali, ambalo jibu lake ni kwamba vitengo hivi kwa sasa havina watumishi wa umma ambao mishahara yao ingepaswa kuonekana hapo, bali kwa sasa wapo Wanajeshi ambao mishahara yao inalipwa kutoka Fungu 38 la Ngome.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni Uteuzi wa Wanajeshi katika nafasi za Kisiasa. Ndugu yangu Naibu Waziri wa Afya amenisaidia kujibu hili eneo, lakini niseme tu hivi kwamba, uteuzi wa viongozi unazingatia weledi na hitajio la uongozi katika eneo husika na kwa kuzingatia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Majukumu ya Viongozi hawa siyo ya kisiasa, bali ni kutekeleza kazi za Kiserikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, uteuzi unaofanywa siyo tafauti na majukumu ambayo Serikali imekuwa mara kwa mara ikiliagiza Jeshi kusaidia mamlaka za kiraia. Kwa maana nyingine, mara kadhaa tumeshaombwa na mamlaka za kiraia kutoa msaada hususan katika maeneo ya mipakani. Kwa hiyo, inaleta mantiki unapomweka Mwanajeshi kusimamaia pale akiwa kiongozi kwa sababu atakuwa na uharaka wa kuchukua hatua kama hizi tunazozizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo baadhi ya Wanajeshi ambao wameteuliwa na Chama Tawala katika nafasi mbalimbali za uongozi. Hata hivyo, uteuzi huo hufanyika kwa makubaliano ya Chama Tawala na Wanajeshi husika baada ya kustaafu utumishi Jeshini na siyo wanapokuwa katika utumishi wa Jeshi. Mfano, uteuzi wa Kanali Lubinga kuwa Katibu wa NEC ya Chama Tawala, ulifanyika baada ya Afisa Mkuu huyo kustaafu rasmi utumishi Jeshini. (Makofi)

Wanajeshi wanateuliwa kushika nafasi za Kiserikali na siyo za kisiasa, hivyo wanaruhusiwa kuvaa sare za Kijeshi kulingana na majukumu na matukio maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ushiriki wa Jeshi katika operation za ulinzi wa amani; napenda niseme kwamba, ushiriki wa Jeshi katika operation za Umoja wa Mataifa umekuwa na faida kubwa hususan kwa kuwawezesha Wanajeshi wetu kuongeza weledi, kuongeza uzoefu na exposure, teknolojia na kuitangaza Tanzania katika tasnia ya ulinzi na usalama duniani. Tumekuwa tukipata sifa nyingi na ni mategemeo yetu kwamba tutaendelea kutuma vijana wetu wakalinde amani katika maeneo mbalimbali duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu eneo la JKT kwamba SUMA JKT limetoa mchango gani kwa Jeshi katika kukabiliana na changamoto za bajeti? SUMA JKT linashiriki kupunguza changamoto za kibajeti kwa Jeshi kwa kuchangia katika uendeshaji wa Kambi na pia kuchangia gharama za chakula kwa vijana JKT ambapo mpaka sasa asilimia 55 ya gharama inalipwa na itaongezeka kufikia asilimia 100 siku zijazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, SUMA JKT kupitia kampuni yake ya ujenzi imekuwa ikishiriki ukarabati na ujenzi wa Kambi na miundombinu bila kutoza gharama ya kazi hizo. Mchango wa SUMA kuipunguzia Serikali gharama za uendeshaji, ni kwamba jukumu la SUMA ni kuipunguzia Serikali gharama za kuendesha JKT. Jukumu hilo limeanza kutekelezwa kwa kuchangia kulisha vijana na gharama za uendeshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi ya miradi ya uzalishaji wa mali wa SUMA JKT, iko mingi ikiwemo kilimo na mifugo, uhandisi wa ujenzi, kutoa huduma za ulinzi kwa jamii, uunganishaji na usambazaji wa matrekta na uzalishaji samani, kokoto na ushonaji wa nguo. Fedha zilizoingizwa kutokana na uzalishaji ni jumla ya Shilingi bilioni 7.8 na zinaonekana katika audit report ya SUMA JKT .

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie eneo hili la Kambi ya Upinzani kwa hoja hii ya Jeshi la Kujenga Taifa, kwamba Jeshi hili ni pamoja na kuwa na dhima ya kuwafunza vijana, kuzalisha mali ikiwemo kuzalisha chakula. Jeshi lipimwe kwa uzalishaji mali na kupunguza njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, JKT lina program ya kuongeza uzalishaji mali na mafunzo ya uzalishaji mali hasa chakula kwa vijana wake kupitia mashamba darasa yaliyopo. Aidha, vijana waliopo kwenye makambi ya JKT wameanza kujitegemea kwa awamu katika gharama za chakula kutokana na chakula wanachokizalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ni nyingi, sitoweza kuzimaliza zote, lakini nataka kuwahakikishia Waheshimiwa kwamba tutazitoa kwa maandishi kabla ya mwisho wa Bunge hili. Kuna eneo moja muhimu sana ambalo limechangiwa na Wabunge wengi, nalo ni migogoro ya ardhi na fidia kwa maeneo ambayo Jeshi limeyatwaa. Eneo hili limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi akiwemo Mheshimiwa Ester Matiko, Mheshimiwa Manyinyi, Mheshimiwa Mabula, Mheshimiwa Deo Sanga na wengi ambao orodha yao ninayo hapa.

Waheshimiwa Wabunge, ninachoweza kusema na naomba mnielewe vizuri kwamba nia ya kulipa ipo, tathmini katika baadhi ya maeneo imeshafanyika, upimaji umeshafanyika, kwa hiyo, kilichobaki ni kulipa tu hiyo fidia inayotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliweka katika bajeti yetu kama nilivyosema shilingi bilioni 27.7, bahati mbaya bado hatujapokea, lakini mazungumzo yanaendelea. Tuna mategemeo kwamba kabla ya mwisho wa mwaka huu wa bajeti, fedha zitakazopatikana tutaanza kulipa fidia zinazotakiwa katika maeneo ambayo nimeyazungumzia hapa. Kwa hiyo, kuna maeneo mengi mno na naweza nikaitoa ile orodha, lakini kwa sababu ya muda, naomba niendelee na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya pensheni ndogo kwa wastaafu waliostaafu zamani. Tunakubaliana kabisa na hoja hii na nataka niseme kwamba Serikali imeanza kulifanyia suala hili ili hatimaye tuweze kurekebisha penisheni hizo. Ila ni lazima tuelewe kwamba wastaafu wako wengi sana na fedha zitakazohitajika ni nyingi sana. Kwa hiyo, lazima zoezi hili liende awamu kwa awamu, ndiyo maana Serikali imeanza na ngazi za juu. Imeanza kutoka cheo cha Meja Jenerali hadi Jenerali kamili na tutaendelea kwa awamu hadi hapo ambapo tutaweza kutimiza jukumu hili la Serikali la kuweza kuwatazama wale ambao wamestaafu muda mrefu uliopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hoja za Mheshimiwa Fakharia, kuhusu idadi ndogo ya wanaojiunga na JKT kutoka Zanzibar. Mpaka sasa hivi wanaojiunga na JKT kwa mwaka tunapeleka nafasi 300. Kila tukiongeza idadi ya wanaoingia JKT, pia tutaongeza idadi ya wale wanaotoka Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawashauri tu Waheshimiwa Wabunge kwamba utaratibu ule wa ugawaji, siyo jukumu la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wala siyo la Jeshi. Tunazikabidhi kwa Serikali ya Zanzibar na kuwataka wao wazigawe kwa kadri watakavyoona inafaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa nilizokuwanazo, kwa sasa zinagawiwa katika Wilaya na Mikoa na kama kuna matatizo huko, likiwemo lile alilozungumzia Mheshimiwa Dau kule Mafia kwamba Mshauri wa Mgambo ndio anachukua watu kutoka nje, hapa naweza kusema kwamba zoezi hili linafanywa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya. Halipaswi kufanywa na mtu mmoja. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Dau kwamba kama ni kweli haya yanatokea, basi ahakikishe anakaa na DC kama Mwenyekiti ili waweze kudhibiti hii hali, kwa sababu suala hili ni jukumu la Kamati ya Ulinzi na Usalama, siyo suala la Mshauri wa Mgambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jasson Rweikiza alitaka kujua tuna-ratify lini ile Biological Weapon Treaty ambayo, tumeshaisaini? Naweza kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati tunaleta hoja hii kwa ajili ya ratification tulipewa ushauri, kwamba kuna treaties nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Chemical Weapons Treaty; kuna Biological Weapon Treaty kuna Nuclear Weapon Treaty; hizi zote ni weapon of mass destruction. Tukashauriwa kwamba ziwekwe kwa pamoja ili ziwe zina sheria moja. Ili ziweze kufanya hivyo, kwa hiyo, tumekubaliana kwamba zoezi hilo sasa lianze kwa haraka ili hatimaye tuweze kui-ratify treaty hii na tuweze kupitisha sheria ili tuweze ku- domesticate sheria zote hizi kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Masoud aliungana na Wabunge wengine kusema kwamba bajeti ya Wizara hii ni ndogo na tunakubaliana na hilo, lakini hiyo ndiyo hali ya uchumi wa nchi. Tuna uhakika kwamba kila uchumi ukikua na Wizara hii itaongezewa fedha kwa umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Ration Allowance kwamba isiondolewe; tunasema kwamba Ration Allowance haijaondolewa; ipo na itaendelea kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la fidia ya maeneo yaliyochukuliwa na Jeshi, nimeshalitolea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ujenzi wa maghala kwamba hayajakamilika na yatakwisha lini? Niseme hapa kwamba maghala yako katika hatua nzuri sana, yaliyobaki ni mambo machache sana ya kuunganisha umeme hapa na pale na kadhalika, isipokuwa lile ghala la Pemba, ambapo kumetokea mgogoro na Mkandarasi. Sasa hivi utaratibu unafanywa wa kuuvunja mkataba ule ili apewe Mkandarasi mwingine mwenye uwezo alikamilishe lile ghala na silaha zetu ziweze kukaa sehemu salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya ulinzi wa Taifa nimeshalitolea taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu eneo la Hospitali za Jeshi kuwa katika mazingira ambayo hayaridhishi na kadhalika. Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia hili. Naweza kusema hapa kwamba tuko katika mchakato wa kuanzisha Bima ya Afya kwa Wanajeshi. Sisi tuna imani kubwa kwamba huo ndiyo utakuwa mwarobaini wa matatizo yote ya kiafya Jeshini. Tutapata fedha za kutosha kuboresha vituo vyetu, kuongeza dawa kuajiri Madaktari na kuwalipa hata wale Madaktari ambao wanakuja kufanya part time. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda wangu umekwisha, bado nina hoja nyingi sana ambazo sijajibu; lakini kama nilivyoahidi, tutazitoa kwa maandishi ili Waheshimiwa Wabunge wote wapate majibu ambayo tulikuwa tumeyaandaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuhitimisha hoja yangu. Nawashukuru wote waliochangia na kusema ukweli nimefarijika sana kwa sababu karibu wote waliochangia wameunga mkono juhudi zinazofanywa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania katika ulinzi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipeke niwashukuru sana Wakuu wa Majeshi Wastaafu ambao wamejumuika nasi katika bajeti hii leo tokea asubuhi na mpaka sasa bado tuko nao. Nawashukuru sana kwa kazi nzuri waliyoifanyia nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji waliochangia kwa maandishi walikuwa 30 na waliochangia kwa kuzungumza walikuwa 17. Hoja ni nyingi, makabrasha ninayo hapa ya majibu karibu yote lakini sina uhakika kama nitapata muda wa kujibu kila hoja iliyotolewa. Kama utaratibu wetu ulivyo, tutatayarisha majibu ya maandishi na kila Mbunge ataweza kupata majibu kwa kadri alivyouliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hoja za Kamati ya Nje, Ulinzi na Usalama. Wao walisema Serikali iongeze ukomo wa bajeti ya Wizara kulingana na mahitaji halisi. Ushauri umepokelewa, Wizara itaendelea kuwasiliana na Hazina ili ukomo wa bajeti uweze kuongezwa na kuiwezesha kukidhi mahitaji halisi ya fedha kwa Mafungu yote matatu yaani Fungu 38, 39 na 57. Namshukuru Waziri wa Fedha kama alivyozungumza siyo kwamba ombi liwe kusiwe na ukomo, hapana, bali ukomo uongezwe ili uweze kukidhi mahitaji ambayo ni ya lazima kwa jeshi letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pia ilisema Serikali itoe fedha zote za maendeleo zilizotengwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 hususani kwa Fungu 38 lililopokea asilimia 41.25 ya bajeti iliyotengwa. Ufafanuzi ni kwamba hadi kufikia mwezi Aprili, 2018 Fungu 38-Ngome limepokea fedha kutoka Hazina kiasi cha asilimia 84.9 ya fedha zilizotengwa kwa mwaka wa fedha 2017/2018 na hivyo Wizara ina imani kuwa Serikali itakamilisha kutoa fedha zilizobaki kwa mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kulikuwa kuna hoja kwamba Suma JKT katika kupunguza tatizo la madeni lijikite kwenye kazi zenye zabuni badala ya kufanya kazi ambazo hazina zabuni na hivyo kupata matatizo katika kulipwa. SuUMAJKT kama zilivyo taasisi nyingine za kibiashara, limekuwa likijikita pia katika kazi zenye zabuni ingawa changamoto kubwa imekuwa ni madeni makubwa hususani kwa taasisi za Serikali. Shirika linatumia mikakati mbalimbali katika kudai madeni kama ifuatavyo:-

(i) Kuwatembelea wateja na kuwakumbusha kulipa madeni yao;

(ii) Kuwaandikia barua wakopaji na wadaiwa na wadhamini kulipa madeni yao;

(iii) Kuwatumia mawakala kudai madeni;

(iv) Shirika limewasilisha orodha ya watumishi wa umma wanaodaiwa madeni kwa Mlipaji Mkuu wa Serikali ili wakatwe kwenye mishahara na pensheni zao;

(v) SUMAJKT limewasilisha orodha ya wadeni wanaodaiwa ili Maafisa Masuuli wawakate kwenye mishahara yao; na

(vi) Kutangaza kwenye vyombo vya habari na kuwafikisha katika vyombo vya sheria mawakala wasio waaminifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa hatua hizi, tunadhani kwamba tutaweza kufanikiwa kwa kiwango kikubwa kupunguza madeni ambayo Suma JKT inaidai taasisi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kulikuwa kuna hoja kwamba Serikali ihakikishe wadaiwa sugu waliokopa matrekta kutoka Suma JKT wanarejesha madeni ya mikopo hiyo inayofikia shilingi bilioni 40. Suma JKT katika kuhakikisha wateja wanalipa madeni yao ya matrekta wamechukua hatua zifuatazo:-

(i) Kuwajulisha wakopaji kulipa madeni yao kwa kuwatembelea;

(ii) Kuwaandikia barua na kutumia vyombo vya habari;

(iii) Kutumia mawakala wa kudai madeni;

(iv) Kuondoa walinzi kwa wadaiwa sugu na kunyang’anya matrekta yaliyo katika hali nzuri kutoka kwa wadaiwa sugu; na


(v) Inaposhindikana wakopaji kufikishwa katika vyombo vya sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hili tatizo la madeni ya matrekta limekuwa sugu, fedha ni nyingi lakini kila hatua itachukuliwa ili wanaodaiwa waweze kulipa madeni yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maslahi ya walinzi SUMA Guard kwamba yaboreshwe, kampuni ya ulinzi binafsi ya SUMAJKT Guard imezingatia viwango vya mishahara ya makampuni ya binafsi ya ulinzi wa ndani. Aidha, inalipa mishahara na marupurupu kwa kiwango kilicho juu ya kima cha chini cha Serikali. Mishahara ya walinzi imepandishwa kwa asilimia 14 kutoka Sh.170,000/= hadi Sh.193,000/= kwa kima cha chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mishahara na marupurupu yameboreshwa kulingana na mazingira ya ngazi na cheo. Hivyo mishahara ya walinzi inaanzia Sh.193,000/= hadi Sh.622,000/=. Aidha, kampuni inakabiliwa na changamoto ya kutolipwa madeni na washitiri wao ambao wengi wao ni taasisi za Serikali hivyo kukwamisha juhudi za kuboresha maslahi kwa watendaji wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ni Serikali itoe fedha shilingi bilioni mbili za maendeleo ambazo hazijatolewa kuwezesha ukarabati wa miundombinu ya kambi za JKT na ujenzi wa kambi mpya ili JKT iweze kuchukua vijana wengi wa mujibu wa sheria kwa mwaka 2018/2019. JKT kwa mwaka 2017/2018 ilitengewa jumla ya shilingi bilioni sita za maendeleo na hadi sasa Serikali imeshatoa shilingi bilioni tano za fedha za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizo zimeleekezwa katika kukarabati na kujenga miundombinu iliyopo katika vikosi na makambi ya JKT kwa lengo la kuliongezea uwezo wa kuchukua vijana wengi kwa mujibu wa sheria na kujitolea. Aidha, JKT kupitia Wizara itaendelea kuwasiliana na Hazina ili kupatiwa kiasi cha shilingi bilioni moja iliyobaki kabla ya kufikia mwisho wa mwaka huu wa fedha ili kukamilisha miradi ya maendeleo iliyopangwa kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ni Serikali itoe fedha za maendeleo kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu katika Mashirika ya Nyumbu na Mzinga. Ufafanuzi ni kwamba katika mwaka huu wa fedha Serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni sita kwa ajili ya Mashirika ya Mzinga na Nyumbu, ambapo Shirika la Nyumbu limepokea shilingi bilioni 2.5 na Shirika la Mzinga limepokea shilingi bilioni 3.5. Tunatarajia kiasi kilichobaki kitapatikana kabla ya mwaka wa fedha kumalizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine Serikali itoe fedha shilingi bilioni 19.8 kwa ajili ya kulipa fidia maeneo ambayo yametwaliwa na jeshi na kipaumbele kutolewa kwa eneo la Rasi Mshind, Kilwa. Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imewasiliana na Hazina na ahadi ya Hazina ni kutoa kipaumbele katika kulipa fidia ya eneo la Rasi Mshindo, Kilwa pamoja na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ikamilishe mchakato wa Sera ya Ulinzi wa Taifa. Serikali imepokea ushauri huu na itaufanyia kazi haraka iwezekanavyo. Jambo hili ni kweli limechukua muda mrefu lakini kama taarifa ilivyotolewa hapa na Mheshimiwa Mbunge mmoja ni kwamba jambo hili limeshakaliwa katika ngazi moja ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na linasubiri hatua zilizobaki kufikia Baraza la Mapinduzi ili hatma ya jambo hili iweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilipe stahili za Majenerali Wastaafu kama zilivyoidhinishwa. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya Majenerali Wastaafu ni shilingi bilioni 3.9 mpaka sasa Wizara imeshapokea kiasi cha shilingi bilioni 2.5 kama Waziri wa Fedha alivyoeleza. Ni matumaini ya Wizara kuwa Hazina itatoa kiasi kilichosalia itakapofika mwishoni mwa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo ndizo zilikuwa hoja zilizotolewa na Kamati, nataka kuishukuru Kamati kwa kazi nzuri wanayofanya za kushirikiana nasi katika kuhakikisha kwamba bajeti yetu inapatikana ili tuweze kutimiza majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine nyingi ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezitoa nitazungumza baadhi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanajeshi wastaafu kukatiwa bima ya afya. Wizara ya Ulinzi kwa kushirikiana na Serikali Kuu inaendelea kukamilisha taratibu stahiki za bima ya afya kwa wanajeshi wote wakiwemo wastaafu pamoja na familia zao. Mpaka sasa tunavyozungumza wanajeshi wanapata huduma za afya katika kambi zao. Kuna zahanati na vituo vya afya katika kambi mbalimbali, kuna hospitali kuu Lugalo na hospitali za kanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kwa sababu za changamoto za kibajeti huduma si vile ambavyo tunataka iwe. Ndiyo maana sasa tumebuni kwamba pengine tuanzishe bima ya afya kwa wanajeshi, tupate pesa ya kutosha, tuboreshe huduma zetu katika vituo vyetu, lakini vilevile tuweze kuwasaidia waliostaafu. Kwa kweli watu waliolitumikia jeshi na nchi yao kwa miaka yote baada ya kustaafu kukosa huduma za afya si jambo la busara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni matumaini yetu kwamba mfuko huu wa bima ukipita, tutakuwa na uwezo wa kutosha kabisa wa kuwahudumia wanajeshi walio kazini pamoja na wale waliostaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya maduka ya bidhaa kufungwa, wanajeshi wapewe exemption ili wapate unafuu katika bidhaa na vifaa mbalimbali. Yupo Mheshimiwa Mbunge nadhani ni Mheshimiwa Selasini alisema kwamba hakuna fidia yoyote iliyotolewa baada ya maduka haya kufungwa. Ukweli ni kama ufuatavyo Mheshimiwa Selasini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maduka ya duty free ya jeshi yalikuwa yana kasoro nyingi. Kasoro moja kubwa ilikuwa ni wale ambao walikuwa wakiyaendesha kuuza bidhaa ambazo hazijalipiwa ushuru nje ya makambi. Hiyo kama vile haitoshi, mimi nimefanya ziara katika kambi nyingi za jeshi, malalamiko makubwa yalikuwa maduka hayo pamoja na kupata exemption ya ushuru bado bei zao zilikuwa kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali imeamua kujipanga ili maduka haya ikiwezekana yaendeshwe na jeshi lenyewe ili tuondokane na kasoro hizo. Wakati huu tuliokuwa nao ambapo bado hatujatengeneza huo uwezo inatolewa fidia kwa kila mwanajeshi ya Sh.100,000/= kila mwezi, kwa hiyo, fidia hiyo ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya usalama wa mipaka ya nchi, Tanzania na Kenya, Tanzania na Uganda, nadhani alikuwa Mheshimiwa Masoud anazungumzia juu ya uwekaji wa mipaka sawasawa. Nakupongeza sana Mheshimiwa Masoud umekuwa ukilifuatilia jambo hili miaka yote lakini nataka kusema kwamba sasa ufumbuzi umeanza kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilizokuwa kwenye mipaka ya Tanzania na Kenya, nchi hizi zimekubaliana kuimarisha alama yaani beacon za mipaka kuanzia Ziwa Viktoria hadi Ziwa Natron na hatimaye kufikia Vanga katika Mkoa wa Tanga. Kazi hii imeanza rasmi tarehe 2 Machi, 2018 ambapo timu ya pamoja ya wataalam imeendelea na kazi kwa awamu ya kwanza kilometa 238. Kazi hii inahusisha pia kuweka beacon za kati ya kila mita 100 na hivyo kufanya mpaka uonekana kwa uwazi na kuondoa utata. Zoezi hili litakamilika kabla ya tarehe 30 Juni 2018. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kuimarisha beacons za mpaka wa Tanzania na Uganda, nayo imeanza ambapo timu ya wataalam wako Mtukula wakiendelea na kazi. Kama ilivyo kwa mpaka wa Kenya beacons za ziada kwenye mpaka wa Tanzania na Uganda zitaongezwa kwenye mstari wa mpaka ili uweze kuonekana kwa urahisi na uwazi. Kwa maana hiyo, kuna mafanikio katika kurudishia mipaka ya nchi zetu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine kwamba Wizara ya Ulinzi na JKT ihakikishe wanakuwa na usafiri wa kutosha kubeba maafisa na maaskari kwenda kazini na kurejea majumbani. Nadhani hii ilikuwa hoja ya Mheshimiwa Lubeleje, Wizara ya Ulinzi na JKT ina utaratibu wa kuwasafirisha maafisa na maaskari kwenda na kurudi kazini nchi nzima. Maafisa na askari hao hupanda magari hayo katika vituo maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, baadhi ya maafisa na askari ambao hutoka mapema kazini kama wanaotoka zamu hukutwa njiani wakisubiri usafiri mwingine. Hata hivyo, juhudi zinafanywa kuongeza magari hayo ili kukidhi hitaji la usafiri kwa asilimia mia katika mikoa na wilaya zote zenye makambi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilikuwa askari iliyepotea baada ya shambulio la tarehe 7 Desemba, 2017. Hii hoja nadhani ni ya Mheshimiwa Yussuf, Umoja wa Mataifa na Serikali kupitia JWTZ wanaendelea na juhudi za kumtafuta askari huyo. Endapo itatimia miezi sita bila askari huyo kupatikana kwa mujibu wa sheria za Tanzania Serikali kupitia JWTZ itaitisha Baraza la Uchunguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa tukio hili, tayari Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ameshaunda Baraza la Uchunguzi ili hatua stahiki zichukuliwe ikiwa ni pamoja na kutoa tangazo la kifo yaani presumed death ili mchakato wa kuandaa taratibu za malipo ufanywe na Umoja wa Mataifa na JWTZ. Huyu kijana amepotea wakati wa shambulio na mpaka sasa hivi anatafutwa, hatuwezi kusema kwa uhakika kama yuko hai au ameshafariki, lakini taratibu ni kama nilivyozieleza hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupate utaratibu wa malipo ya stahiki kwa wanajeshi wanaofariki au kuumia wakiwa katika operesheni za ulinzi wa amani. Wanajeshi wanapoumia au kufariki wakati wakiwa katika majukumu ya ulinzi wa amani malipo yake yanatolewa katika sehemu mbili. Sehemu ya kwanza hutolewa na Umoja wa Mataifa na sehemu ya pili hutolewa na Serikali yetu kwa kuzingatia kanuni za pensheni katika majeshi ya ulinzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zinazotolewa na Umoja wa Mataifa ni kwamba, mwanajeshi akiumia katika jukumu la ulinzi hulipwa baada ya kufanyiwa Bodi ya Tiba yaani Medical Board na hulipwa baada ya kujaziwa nyaraka muhimu. Malipo haya hufanyika kwa kuzingatia kiwango cha kuumia. Mwanajeshi akifariki Umoja wa Mataifa hutoa dola za Kimarekani 70,000 ikiwa ni rambirambi kwa familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa Umoja wa Mataifa umetoa fedha zote kwa askari wetu waliofariki katika majukumu ya ulinzi wa amani na wote wamelipwa isipokuwa kwa wale ambao taratibu za mirathi bado hazijakamilika. Wizara inaomba kushauri kuwa familia ambazo hazijakamilisha taratibu za mirathi zikamilishe haraka iwezekanavyo ili wahusika walipwe fedha zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanajeshi akifariki, Serikali hutoa fedha zifuatazo:-

Fedha za rambirambi ambazo hutolewa na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ikiwa ni mshahara wa mwanajeshi wa miezi sita; kusafirisha familia na mizigo ya marehemu kwenda nyumbani na hutoa death gratuity pamoja na survivor pension. Kwa hiyo, katika suala hili hakuna utata hata kidogo, fedha hizi zinapatikana bila ya tatizo lolote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzalishaji mali. Jeshi lichukue hatua za kuimarisha tafiti kwa ajili ya matumizi ya kijeshi na kiraia. Ushauri umepokelewa, hata hivyo, ili kuimarisha utafiti Serikali inaendelea na hatua za kuboresha utendaji wa mashirika ya Mzinga, Nyumbu na SUMA JKT kwa kuwapatia rasilimali watu, fedha na ukarabati wa miundombinu pamoja na vitendea kazi.


Mheshimiwa Mwenyekiti, kutolipwa kwa madeni ya SUMAJKT yakiwemo madeni ya matrekta na SUMA Guard, hili nimeshalizungumizia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, SUMA JKT vifaa vyake vya ujenzi na ulinzi ni duni Serikali iwawezeshe. SUMAJKT imekuwa ikiendelea kujiimarisha kivifaa kadri ya mapato yake yanavyoruhusu. Kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018, shirika limenunua mitambo nane mbalimbali ya ujenzi ili kukiwezesha kitengo chake cha ujenzi na kampuni ya ulinzi kufanya kazi kwa ufanisi. Aidha, kupitia kampuni yake ya ulinzi limenunua vifaa vifuatavyo:-

Gari la zimamoto na uokoaji kwa ajili ya shughuli za zimamoto; magari matano kwa ajili ya kuimarisha shughuli za doria katika malindo yake; mitambo ya kisasa ya CCTV Camera na kujenga control room. SUMA JKT Guard litaendelea kuboresha zana, mitambo na vifaa vya utendaji kadri mapato yake yatakavyoruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu operesheni za jeshi na mahusiano na mamlaka ya kiraia. Kulikuwa na hoja kwamba wanasiasa wasilitumie JWTZ kwa shughuli za kisiasa ndani ya nchi. JWTZ halijawahi kutumiwa kisiasa na wanasiasa. JWTZ linatumika kutekeleza majukumu kwa mujibu wa sheria na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja nadhani Mheshimiwa Waitara kwamba jeshi lilitumika wakati wa uchaguzi Zanzibar. Hili nililijibu mwaka jana na naomba nilirudie, tutofautishe kati ya jeshi kutumika wakati wa uchaguzi na jeshi kulinda major installations wakati wa uchaguzi. Wakati wa uchaguzi kwa taarifa zenu Waheshimiwa vyombo vyote vya ulinzi na usalama vinakuwa standby. Jeshi wakati mwingine linatumika katika kulinda major installation isitokee uhujumu. Zanzibar jeshi lilinda airport, bandari na maeneo ya kuzalisha umeme. Huko siyo kuingilia uchaguzi, kwa hiyo, jeshi halitumiki kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, JWTZ itoe msaada wa kiutendaji polisi. Jibu ni kwamba kulingana na mgawanyo majukumu ya ulinzi na usalama wa nchi yetu jukumu la usalama wa raia na mali zao ni jukumu la polisi. Hata hivyo, endapo kutatokea hitaji la kushirikisha vyombo vingine vya ulinzi na usalama, JWTZ hutoa msaada huo kwa kuzingatia Sheria ya Ulinzi wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uhusiano huo mzuri, nchi yetu imeendelea kuwa salama. Tunachosema hapa ni kwamba jeshi lina jukumu la kutoa msaada kwa mamlaka za kiraia na vyombo vingine vya ulinzi na usalama wanapohitajika kufanya hivyo. Kwa hiyo, pale ambapo polisi wanahitaji msaada wa jeshi zipo taratibu za kufuata na jeshi huwa wanatoa msaada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matishio ya ugaidi. Kumekuwepo na viashiria vya ugaidi nchini Tanzania na hitajio la military intelligence kusaidia jeshi la polisi. Yapo matukio yenye viashiria vya ugaidi ambayo yamekuwa yakijitokeza nchini. Jeshi la Polisi limekuwa likikabiliana matukio hayo kwa mafanikio makubwa na kuweza kuyadhibiti. Aidha, vyombo vya ulinzi na usalama vina utaratibu wa kubadilishana taarifa ya kiutambuzi kuhusiana na matishio mbalimbali ikiwemo ugaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo kikubwa cha Kupambana na Ugaidi (National Counterterrorism Center) kinachojumuisha vyombo vya ulinzi na usalama kinakusanya taarifa za utambuzi kuhusiana na ugaidi na kuzifanyia kazi kwa pamoja. Matishio ya hivi sasa yanavifanya vyombo vya ulinzi na usalama kufanya kazi kwa ukaribu sana na kwa kweli mafanikio makubwa yamepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya Mheshimiwa Abdallah Bulembo kwamba Serikali iwaajiri vijana wa JKT walioshiriki ujenzi wa ukuta Mererani. Nadhani jibu lake limeshatolewa na Mheshimiwa wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya vijana wa mujibu wa sheria iongezwe ili ichukue vijana wengi. Hili linafanyiwa kazi, sasa hivi tumeongeza kambi za JKT katika maeneo kadhaa lengo ni kuongeza vijana wanaochukuliwa kwa mujibu wa sheria na wale wa kujitolea ili wale wote wanaomaliza form six kabla ya kujiunga na vyuo vikuu waweze kujiunga na jeshi angalau kwa kipindi kifupi waweze kupata yale ambayo yamekusudiwa katika jukumu hili la kujiunga na JKT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kidogo kuhusu vijana wa JKT na malalamiko yao kuhusu ajira. Hapa ni vyema nikalieleza hili kwa kina kidogo ili lieleweke. Vijana wanaokwenda JKT kwa kujitolea sasa hivi wamezidi kuongeza sana na sababu ni kwamba wanadhani ndiyo njia ya kupata ajira. JKT imekuwa ikitoa ufafanuzi na mimi napenda niurudie hapa, kwamba kujiunga na JKT kwa kujitolea hakukupi uhakika wa kuajiriwa na vyombo vya ulinzi na usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanaobahatika wachache, wataajiriwa na wale ambao hawapati nafasi za ajira watapewa stadi za kazi ili wanapotoka JKT waweze kujiajiri wao wenyewe. Hili ndilo lengo na miezi sita ya kwanza wanafundishwa mafunzo ya kijeshi na baada ya hapo wanafundishwa stadi za kazi ili hatimaye wale wanaokosa ajira waweze kujiajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vyema Waheshimiwa Wabunge wakati wa usaili wa vijana wanaojiunga na Jeshi la Kujenga Taifa katika wilaya zetu watambue hilo. Maana wao wanadhani watu 5,000 wote wataingia katika jeshi hili sio jambo ambalo linawezekana kwa sababu inategemea na idadi ya nafasi za ajira zinazotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia kwamba sasa hivi tunafarijika sana kwamba vyombo vyote vya ulinzi na usalama kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ajira zinafanyika kupitia JKT. Polisi, Magereza, Uhamiaji, Usalama wa Taifa, Jeshi lenyewe na vyombo vingine vyote vya ulinzi na usalama wanachukua vijana kutoka JKT kwa ajili ya ajira katika vyombo hivyo. Bado vijana wanaojiunga na JKT ni wengi mno kuweza wote kupata ajira. Kwa hiyo, tunaendelea kusisitiza kwamba vijana hawa wawe tayari kujifunza stadi zile wanazopewa ili hatimaye waweze kwenda kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna migogoro mingi ya ardhi ambayo Waheshimiwa Wabunge wameizungumzia kati ya jeshi na wananchi. Nitaizungumzia baadhi, kwanza, Serikali ishughulikie mgogoro wa ardhi kati ya Kambi ya JKT Itaka na vijiji jirani. Kambi hii ilirithi eneo lililokuwa shamba lililokuwa Maganga Estate ambalo lilikuwa limepimwa kwa muda mrefu na kukabidhiwa kwa JKT. Hii ni hoja ya Mheshimiwa Haonga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuonekana dhahiri kuwa wananchi wamevamia eneo kubwa la kikosi kulifanyika upimaji upya na kupunguza eneo la shamba la JKT kwa wananchi. Kwa mgogoro huu uliotajwa na Mheshimiwa ni dhahiri kuwa wananchi wamezidi kuvamia maeneo ya kikosi. Timu ya wataalam kutoka Wizara ya Ulinzi na JKT, itaenda kufanya tathmini ya hali ya uvamizi na kushauri nini kifanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo mengine ya migogoro ya ardhi kwa mfano katika eneo lile la Mheshimiwa Esther Matiko, anataka kwamba JWTZ ilipe fidia ya ardhi iliyotwaliwa la sivyo irudishe ardhi kwa wananchi. Tunasema kwamba eneo linalotumiwa na JWTZ la Nyamisangura lilitwaliwa kwa kufuata taratibu za Sheria ya Ardhi ikiwa ni pamoja na kufanya upimaji na uthamini kwa ajili ya fidia. Eneo hili lina ukubwa wa hekta 123.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uthamini wa mali za wananchi ulifanywa mwaka 2015 na kiasi cha shilingi bilioni 1.5 zilitakiwa kulipwa kwa wananchi 204 kama fidia. Ahadi ya Serikali ni kulipa fidia kwa mujibu wa Sheria za Ardhi zilizopo kwa kuzingatia thamani ya sasa ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu eneo la Rasi Mshindo kule Kilwa, hili nilishalizungumzia kwamba tunajipanga ili fedha za fidia zitakazopatikana ziweze kulipa fidia katika eneo hili ili iundwe ile base ya navy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi ya Jeshi Mtoni Zanzibar siyo nzuri kiusalama, imevamiwa na shughuli za kibiashara kama vile maduka, bar na sehemu za kuoshea magari. Je, shughuli hizi ni za Jeshi? Eneo hili la Kambi ya Jeshi Kikosi cha 111 Mtoni kabla ya ujenzi wa uzio na vibanda vya biashara lilikuwa likitumiwa na watu ambao ni waovu. Hivyo uwepo wa shughuli hizo za kibiashara unasaidia kuimarisha ulinzi na usalama wa eneo hilo. Shughuli hizo zinaratibiwa kikamilifu na jeshi lenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hoja ya Mzinga kwamba shirika lijikite zaidi katika maeneo ambayo wanaweza kufanya kwa ufanisi mfano shirika lilipewe kazi ya ujenzi wa barabara katika Wilaya ya Malinyi, Morogoro na walishindwa kufanya kazi hiyo kwa ubora na kwa muda uliopangwa. Miradi ya barabara ya Malinyi ilisainiwa Machi, 2016 na ilitakiwa kukamilika Juni, 2016. Kazi ilipoanza ilikumbwa na kipindi cha masika ikabidi zisimame kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika ulipoombwa muda wa ziada mteja ambaye ni Halmashauri ya Malinyi aliamua kusimamisha kazi, vifaa vyote vinavyotakiwa kwa barabara ya kiwango cha moramu vilikuwepo eneo la kazi. Kampuni ya Mzinga Holding imetekeleza miradi mingi vizuri kama Halmashauri ya Mkalama, Ikungi na Hospitali ya Manispaa ya Morogoro. Hiyo ni mifano michache kati ya miradi mingi iliyotekelezwa vizuri kwa ubora na ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kuhakikisha karakana ya Nyumbu inaimarishwa hadi kuunda magari yake ukiacha matengenezo ya kawaida na uchongaji wa vyuma. Ushauri huu umezingatiwa, shirika kwa kushirikiana na wadau limeandaa mpango wa maendeeleo wa miaka 10 wenye azma ya kuliimarisha. Mpango umelenga kulirejesha shirika kwenye lengo la kuanzishwa kwake ikiwa ni pamoja na utengenezaji wa gari la Nyumbu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine ya mradi ya matrekta ambayo nadhani nilishauzungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hii hoja ya wanajeshi 19 waliouwawa Congo DRC na wengine kujeruhiwa, je, ni lini watarejeshwa? Nadhani hoja hapa Mheshimiwa Mbunge alisema kuna uzembe mkubwa; hawana zana zinazotakiwa na hawakupata msaada kwa sababu ya uzembe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii nimwarifu Mheshimiwa Mbunge pengine ni vyema kabla hajatoa hoja zake Bungeni angekuja kuonana na mimi nikampa taarifa. Mimi mwenyewe nilikwenda Congo baada ya ajali hii, niliona na niipata maelezo ya kina na najua mambo yote yaliyotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa ya Mheshimiwa Mbunge, kule kuna Brigedi inayoitwa Force Intervention Brigade (FIB) inaundwa na nchi tatu: Tanzania, Malawi na Afrika ya Kusini. Kila kikundi kati ya vikundi hivi vya nchi tatu kina uwezo wake tofauti. Wenzetu wa South Africa wana uwezo wa mapigano ya ndege, kwa hiyo helkopta ni za South Africa, Watanzania na Malawi wana zana za aina nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilipotokea ambush hii kwa sababu eneo hilo ni mbali ililazimika ndege zitumike jambo ambalo halikufanyika. Kwa hiyo, kusema uzembe wa Watanzania au kwa sababu kikosi chetu hakina silaha za kutosha ni makosa. Ningependa Mheshimiwa Mbunge wakati mwingine anione ili nimpe taarifa kwa sababu kauli kama hizi hazifai kutolewa ndani ya Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimweleze vilevile Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeunda Tume ya Uchunguzi na imeshatoa taarifa yake. Kama nilivyosema katika hotuba yangu leo asubuhi, wadau wote wakiwemo Umoja wa Mataifa, nchi hizi ambazo zinaundwa Brigade hiyo ya FIB pamoja na ule uongozi wa MONUSCO, kila mtu atachukua hatua stahili kuhakikisha kwamba matukio kama haya hayatokei tena. Kwa hiyo, wanapokwenda watu katika operesheni ajali huwa zinatokea, hili tulielewe. Kwa hiyo, kusema kwamba ni uzembe kwa kweli hii siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu stahili za wanajeshi, juhudi za Wizara za kuwapatia wanajeshi wetu makazi bora ziendelee kwa lengo la kuwapatia wanajeshi makazi bora na yenye utulivu. Ukweli ni kwamba kweli bado wanajeshi wengi wako uraiani, lakini Serikali imefanya juhudi kwani tumejenga nyumba 6,064 ambazo lengo lake lilikuwa ni kupunguza wanajeshi wanaokaa uraiani warudi makambini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kila sababu ya wanajeshi kurudi makambini kwa sababu pamoja na mambo mengine nidhamu lakini vilevile wanapohitajika waweze kupatikana haraka. Kwa hiyo, Serikali itaendeleza juhudi hizi za kutafuta fedha kwa ajili ya kuendelea kujenga makazi ya wanajeshi kwenye makambi ili hatimaye wanajeshi wote warudi katika makambi, lakini hii itategemea sana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo ya stahili kwa wanajeshi walioshiriki Operesheni Kibiti kama wamelipwa stahili zao zote na kiwango walicholipwa kama kinafanana na kile walicholipwa wenzao wa TISS na Polisi. Askari walioshiriki katika Operesheni Kibiti wote wameshalipwa stahili zao kwa mujibu wa taratibu za JWTZ. Aidha, kila taasisi ina utaratibu wake wa malipo inapokuwa kwenye jukumu fulani. Hivyo ni vyema ieleweke kwamba jeshi limelipa kwa taratibu zake na kwa maana hiyo halipaswi kulinganishwa na taasisi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mishahara ya wanajeshi kuongezwa na posho zao pia zipatikane, ninachoweza kusema ni kwamba mishahara ya wanajeshi inaongezwa mwaka hadi mwaka kwa kadri fedha za bajeti zinavyoruhusu. Napenda pia niseme kwamba posho zao zinapatikana, wanajeshi wanapata posho zao, ni kweli kwamba wangependa ziongezeke na sisi sote tunapenda iwe hivyo, lakini hili linategemea sana uwezo wa Serikali. Nataka niwahakikishie kwamba uwezo wa Serikali utakapoongezeka basi kila mara posho zao zitakuwa zinaongezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya kwamba matukio mengi yanayoashiria vitendo vya ugaidi yanaongezeka nchini na kwamba sasa litumike jeshi kudhibiti vitendo hivyo. Kama nilivyosema awali ni kwamba kumekuwepo na matukio kadhaa yenye viashiria vya ugaidi nchini na matukio haya yamesababisha vifo, majeruhi na hofu kwa wananchi. Hata hivyo, matukio haya yamekuwa yakidhibitiwa na Jeshi la Polisi, JWTZ limeendelea kujizatiti kukabiliana na matukio yote ya kigaidi endapo litahitajika kushiriki kama ilivyofanya katika Operesheni iliyotokea pale Kibiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira, Mheshimiwa Halima Mdee kwa ufupi anachojaribu kusema ni kwamba hawa vijana wanaojiunga na JKT wapate ajira. Kama nilivyosema awali tutaweza kuchukua baadhi yao, haiwezekani wachukuliwe wote kwa sababu idadi ya wanaojiunga ni wengi mno na vyombo vingine vya ulinzi na usalama vitafanya hivyo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iongeze muda wa mafunzo kwa mujibu wa sheria ili kuwajengea vijana uwezo wa kujifunza zaidi stadi za kazi. Mabadiliko ya muda wa mafunzo kwa vijana kwa mujibu wa sheria ni suala mtambuka kwani limechangiwa na mabadiliko ya mihula ya masomo ya kujiunga na elimu ya juu. Hata hivyo, wadau wa pande zote wanaendelea kukutana ili kuona namna nzuri itakayopelekea vijana kupata mafunzo kwa muda stahiki na kunufaika na mafunzo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana nyingine ni kwamba sasa hivi vijana wanaomaliza form six wanachukuliwa kwa awamu kwa muda wa miezi mitatu tu ambayo na sisi tunakiri kwamba pengine haikidhi haja. Ni vyema muda huu ukaongezeka lakini utaingiliana na muda wa kujiunga na vyuo vikuu. Ndiyo maana wadau wameanza kukaa na wataendelea kukaa ili kuweza kupata ufumbuzi wa jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu makambi ya JKT kuwa machakavu na kwamba Serikali iongeze juhudi za kuyaboresha, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea kuboresha makambi haya. Kama tulivyosema kwamba fedha za mwaka huu wa bajeti tayari shilingi bilioni tano zimekwishapatikana na kazi hiyo inaendelea kwa kuboresha na kuanzisha makambi mapya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu wa vijana kusailiwa kujiunga na JKT, Wabunge wanatoa hoja kwamba pengine utaratibu siyo mzuri na wanaiomba Makao Makuu ya JKT waende hadi ngazi ya wilaya ili kuepusha upendeleo. Malalamiko haya tumeshayapata mara nyingi na tutautazama upya utaratibu huu lakini lazima niseme hapa na hili ni pamoja na Zanzibar, kulikuwa kuna hoja kutoka Zanzibar kwamba utaratibu tunaotumia wa kuchukua vijana kwenda JKT siyo mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kusema ni kwamba jukumu la utaratibu gani utumike kwa Zanzibar ni la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Sisi tunapelekea nafasi hizo katika Serikali ya Mapinduzi na wao kwa mujibu wa taarifa nilizokuwa nazo mimi wanazigawa katika wilaya zao ili tuweze kupata vijana katika wilaya zote. Sasa kama kuna kasoro, basi nitawaomba Waheshimiwa Wabunge tusaidiane kufikisha taarifa hizi kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ili wao wapange vizuri zaidi jinsi ya kuchukua vijana kutoka kule lakini hatuwezi kuliingilia sisi kwa sababu tukishawafikishia nafasi zao hilo ni jukumu la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupanga mchakato huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wa Bara, nimepata malalamiko vilevile kwamba kuna upendeleo. Baadhi ya wilaya vijana wa wilaya zile hawapati wanapata kutoka nje ya wilaya. Taarifa nilizokuwa nazo mimi ni kwamba jambo hili halifanywi na mtu mmoja linafanywa na Kamati ya Ulinzi na Usalama. Ni vyema basi tukahakikisha kwamba Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya zinahakikisha kwamba nafasi zinazotolewa kwa kila wilaya ni vijana wa wilaya husika tu ndiyo wanapata nafasi hizo. Tutapeleka wawakilishi wa Makao Makuu ya JKT ili tuweze kuhakikisha kwamba utaratibu huo unafuatwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kengele ya kwanza imeshapigwa, sasa nimalizie tu, kuna hoja ilitolewa kwamba wanajeshi wanakatwa fedha za chakula wanapokuwa katika mafunzo na pia wanalipia huduma za umeme, nadhani lilitolewa na Mheshimiwa Maryam Msabaha. Nadhani hii taarifa aliyokuwa nayo Mheshimiwa Maryam siyo sahihi. Wanajeshi wanapewa ration allowance na wanapokwenda kwenye mafunzo kwa sababu ration allowance zao wanazo wanatakiwa kujilipia chakula, lakini ni si kweli kwamba wanalipa umeme, umeme bado unalipwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pengine hoja hapa ilikuwa ni kwamba watu wapate ration allowance zao na wanapokuwa kwenye mafunzo walishwe. Hili tunasema kutokana na tatizo la kibajeti tumeona ni vyema kwa kuwa ration wanapata basi waweze kujilipia wao wenyewe na Serikali itaendelea kuwalipia wale ambao wako kwenye operesheni. Ukiwa kwenye operesheni kwa sababu hakuna mzabuni kule lazima Serikali ikulishe wakati huo huo fedha zako za ration zinaingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa hoja ya Mheshimiwa Yussuf ambayo anasema hakuna amani katika nchi yetu. Naomba nimsihi sana, mimi nadhani tuko hapa leo tunazungumza na Watanzania katika nchi hii tunajivuna kwamba katika nchi zinazotuzunguka yenye amani peke yake ni Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kusema kwamba Tanzania haina amani siyo sahihi hata kidogo. Mipaka yetu yote iko shwari kama nilivyosema katika hotuba yangu na ndiyo maana Tanzania tuna amani na watu wanafanya kazi na maendeleo yanaonekana. Ndugu yangu ukienda nchi za jirani zetu Burundi, Congo, Somalia kote huku kuna matatizo makubwa sisi hatupaswi kusema hatuna amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimesema katika hotuba yangu vilevile kwamba changamoto hazikosi, wapo wahalifu, wapo wanaoingia kwetu na silaha kutoka katika nchi zao, changamoto zipo. Wapo wanaowabughudhi wavuvi wetu katika mito na bahari, changamoto hizo zipo, lakini tuzichukulie kama changamoto ambazo vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vinafanya kazi kuhakikisha kwamba tunaziondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla nchi yetu ina amani na mimi nataka nichukue fursa hii nilipongeze Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na vyombo vyote vya ulinzi na usalama kwa kazi nzuri sana wanayoifanya ya kuilinda nchi yetu. Nawaomba waendelee na moyo, uzalendo na weledi wao huo ili nchi yetu iendelee kuwa na amani tuweze kusonga mbele katika maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, naomba kutoa hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuja kuhitimisha hoja yangu jioni ya leo. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha, kutupa afya njema ili kuweza kuhitimisha majukumu ya Wizara yangu kama ambavyo ilivyo ada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii kwa kuzungumza na kwa maandishi. Waliochangia kwa maandishi idadi yao ni 29 na waliochangia kwa kuzungumza idadi yao ni 15 ukiwajumuisha Mheshimiwa Mwakyembe, Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Waitara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kujibu hoja kwa hoja za Kamati; kwa kiwango kikubwa Kamati imejielekeza katika kuiombea Wizara ya Ulinzi iweze kupata fedha za kutosha kutekeleza majukumu yake. Tunashukuru kwa hilo na hatuna shaka yoyote kwamba kadri hali ya uchumi inavyoimarika Serikali inaona umuhimu wa kuongeza fedha kwa Wizara yetu ili majukumu yetu ambayo ni ya msingi kabisa ya ulinzi wa nchi yaweze kufanyika kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo Kamati ya NUU (Nje, Ulinzi na Usalama) imeshauri kuongezwa kwa ukomo wa bajeti ya Wizara ya Ulinzi, Serikali ione umuhimu wa kuongeza kasi ya ulipaji madeni ya kimkakati kwa kutenga fedha zaidi kwenye miradi ya maendeleo, Serikali itoe fedha za maendeleo zilizoidhinishwa kwa Fungu 38 kwa mwaka wa fedha unaoisha, Serikali ione umuhimu wa kuongeza fedha za maendeleo zilizotengwa, Serikali itoe fedha zote zilizoidhinishwa kwa ajili ya kugharamia mafunzo na usalama na utambuzi, Serikali itoe fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya utunzaji wa zana, magari, mitambo na Serikali itoe fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya kuboresha mfumo wa mawasiliano salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla karibu hotuba nzima ya Kamati ilijikita katika uona umuhimu wa kuweza kupata bajeti stahili ya kutekeleza majukumu yetu na sisi tunasema ahsanteni sana na Serikali kwa kweli nia hii ipo, kadri uwezo unavyoongezeka na Wizara hii inaweza kupata mgao unaostahili kwa majukumu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hao, naomba sasa niingie kwenye hoja za Kambi ya Upinzani na nianze kwa kusema leo nimesikitishwa sana kwa kauli zilizokuwa zinatolewa kuhusu Jeshi letu. Tumezoea kusikia kwamba ndani ya Bunge hili kila mtu anaunga mkono kazi nzuri zinazofanya na Jeshi letu. Yanapotokea maneno aidha ya kukashifu au kukejeli kwa kweli huwa napata taabu sana kwa sababu Waheshimiwa Wabunge, sisi sote ni mashahidi juu ya kazi nzuri inayofanywa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuangalie tu majirani zetu wapi kuko salama kama tulivyo sisi. Sasa tusichukulie kwamba amani hii tuliyokuwa nayo ipo tu imekuja yenyewe, kuna watu wanafanya kazi usiku na mchana. Kwa hivyo, naomba niwasihi sana ndugu zangu katika suala la ulinzi wa nchi tusiingize sana siasa. Tukiingiza siasa tutaharibu kwa sababu ulinzi ndiyo kila kitu. Bila ya ulinzi, bila ya amani hamuwezi kufanya kingine chochote. Kwa hiyo, bila shaka tutarekebisha kauli zote zilizotolewa ambazo kwa kweli hazikuwa na sababu ya kutolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hili la hali za wanajeshi wastaafu hususan cheo cha private hadi Brigadier General hazilingani na uzito wa kazi wanazozifanya. Niseme tu Serikali inathamini kwa kiwango kikubwa kazi zinazofanywa na zilizofanywa na wanajeshi wastaafu. Serikali imehakikisha wanalipwa mafao yao ya kustaafu kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo za utumishi wa JWTZ. Aidha, Serikali imeendelea kupitia upya mafao ya wanajeshi wastaafu wote ili aweze kuendelea kulipwa kwa kuzingatia hali ya uchumi ilivyo kwa lengo la kuboresha maslahi haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilieleze Bunge lako tukufu kwamba mpango wa kuboresha maslahi kwa wanajeshi wanaostaafu upo na tunaenda hatua kwa hatua, Jeshi hili ni kubwa. Huwezi kufanya watu wote wapate mara moja. Ilianza ngazi ya Major General mpaka Jenerali, itafuata ngazi nyingine na hatimae tutakamilisha Jeshi lote lakini maadam nia na dhamira ipo, hali ya uchumi ikiruhusu jambo hili litatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja kutoka Kambi ya Upinzani kwamba nyongeza ya mishahara kwa wanajeshi, wao waliita annual increment haipo kwa maana walisema wanajeshi hawapati annual increment kwa kipindi chote cha Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaeleze kwamba statement hiyo sio kweli, Serikali inaendelea kutoa annual increment kila mwaka kwa ngazi za vyeo husika. Serikali imekuwa ikitoa nyongeza za mishahara kwa maana annual increment kwa kipindi chote cha Serikali ya Awamu ya Tano na inaendelea kufanya hivyo. Aidha, hakuna malimbikizo yoyote ya annual increment ambayo hayajalipwa au wanajeshi wanadai. Pia hakuna posho zilizofutwa, bali zilizopo zimeendelea kuboreshwa zaidi mfano, kwa mwaka wa fedha 2018/2019 posho za wanajeshi zimeboreshwa kwa asilimia 15 ikilinganishwa na posho za mwaka uliopita. Kwa hiyo, hapa tunachozungumzia ni kwamba kila mwaka kwa kila cheo kuna increment wanayopata kwenye mishahara yao. Lakini vilevile posho zinazotolewa kwa mfano Ngome Allowance ile ya makazi fedha za maji, fedha za umeme, fedha za taaluma zote zimekuwa zikipata increment na kama nilivyosema kwa kiwango cha asilimia 15. Kwa hiyo, ningeomba sana kwamba hizi statement zinazotolewa pengine ni vyema watu wakathibitisha kabla ya kuzisema ndani ya Bunge lako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu posho ya chakula kwa wanajeshi yaani ration allowance, Kambi ya Upinzani imesema imegeuzwa kuwa ada ya kulipia mafunzo katika shule na vyuo vya kijeshi kwa wanajeshi wanaokwenda mafunzoni. Nataka niwaeleze ndugu zangu kwamba ration allowance ni fedha zinazotolewa kwa ajili ya kumlisha mwanajeshi na kila mwanajeshi anapata fedha hizo kupitia kwenye akaunti yake pamoja na mshahara wake. Kwa hiyo ukisema kwamba umepewa fedha za chakula halafu umekwenda kwenye mafunzo unataka ulishwe, hiyo sio sawa. Cha msingi hapa ni kwamba kuna maeneo machache ambayo watu wanaopata ration allowance bado wanapewa na chakula, nayo ni katika operations, siyo kwenye mafunzo ya kawaida. Kwa hiyo, operations na kazi za mipakani, kule wanalishwa na wanapata ration allowance, lakini kwa wengine wote wanatakiwa wajilishe kwa sababu fedha hizo wameshaingiziwa kwenye akaunti zao. (Makofi)

Kuhusu suala la JWTZ kuingilia utendaji wa kazi za Jeshi la Polisi, mimi nadhani tu niliweke sawa hili ili Waheshimiwa waelewe, vyombo hivi vya ulinzi na usalama haviwezi vikafanya kazi kila kimoja peke yake, hiyo itakuwasiyo kazi ya ulizi. Kazi ya ulinzi inataka vyombo vishirikiane, kwa sababu matishio ni tofauti. Unaposema kwamba jeshi la wananchi libaki mipakani, wakati kuna ugaidi, unategemea itakuwaje. Inapokuwakuna suala la ugaidi lazima Jeshi la Polisi, Jeshi la Wananchi, Usalama wa Taifa na vyombo vingine vya ulinzi na usalama vishirikiane, ndicho kinachoanyika. (Makofi)

Kwa hiyo, JWTZ na Jeshi la Polisi ni Vyombo vya Ulinzi na Usalama ambavyo vimeundwa kwa sheria na mipaka ya majukumu yao ya kiutendaji ipo wazi, na hakuna mwingiliano wowote. JWTZ itanedelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria za nchi yetu na bila kuingilia mamlaka ya vyombo vingine vya ulinzi na usalama, ni masikitiko na bahati mbaya sana kwa Kambi ya Upinzani kudiliki kusema, kuwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi anaingilia Mamlaka ya Jeshi la Polisi, hii siyo sahihi, hata kidogo na tunaikataa kwa nguvu zote, kwa sababu kwanza tutambue kwamba Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, ndiyo Mwenyekiti wa Kamati ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama. Kwa hiyo, Mkuu wa Majeshi anayo haki kuzungumzia vyombo vyote kwa ujumla wake, akiwa kama Mwenyekiti. (Makofi)

Kwa hiyo, nadhani hoja hii siyo sahihi na tuendelee kuamini kwamba bila ya kuwa na Jeshi kushirikiana na vyombo vingine, kuna baadhi ya kazi zitashindikana kufanyika! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kwamba Serikali haiwekezi kwenye shughuli za ugunduzi na utafiti katika JWTZ. Nataka niwaeleze ndugu zangu kwamba ukienda Nyumbu, ukienda Mzinga, utakuta kuna baadhi ya tafiti zinafanyika hadi leo, ni kweli tunakiri kwamba fedha za kuwawezesha kufanya tafiti kubwa bado hazijapatikana, lakini hii haikuwakatisha tamaa, wamekuja na mpango mkakati, taasisi zote mbili hizi; Nyumbu, wao wamekuja na mpango wa miaka 10, wenye bajeti ya shilingi bilioni 227 na kwa miaka mitano ya kwanza bilioni 105. Fedha hizi zikipatikana kupitia bajeti zetu kwa sababu sasa hivi hili suala liko katika majadiliano Serikalini, Shirika hili litaweza kufanya kazi zake za utafiti inavyotakiwa na vilevile Mzinga wana mpango wa miaka mitano, wenye bajeti ya shilingi bilioni 152 ambao na wenyewe fedha hizi zikianza kutiririka katika bajeti zao kwa miaka inayokuja, wataweza kufanya tafiti kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mchakato wa manunuzi ya sare za Jeshi, kwamba uchunguzwe. Walisema Kambi ya Upinzani, kwamba taratibu za ununuzi wa mavazi ya Jeshi hufuata taratibu kwamba hauendi, yaani una walakini, lakini pia wanajeshi wanavaa mavazi ambayo hayawatoshi, kwamba kuna mavazi madogo au makubwa wanapewa. Sasa tuweke sawa kwanza kuhusu mchakato wa manunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna utata wowote katika utaratibu wa manunuzi ya mavazi ya Jeshi. Tender zinatolewa kama kawaidia, watu wanashindanishwa kama kawaida na wanaoleta mavazi hayo basi wanakuwa wamweshinda kitaratibu zinazohusika, sasa sijui Kambi ya Upinzani wanalitoa hili wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu mavazi kutowatosha wavaaji, nalo ni maelezo ambayo yana kasoro. Niseme tu kwamba mavazi yote ya Jeshi, yote, wanajeshi kila mtu anapimwa isipokuwa kombati, kwa hiyo, ukiwaonaleo wanajeshi wote wamevaa mavazi yanayowatosha, kwa sababu wanapimwa. Kombati peke yake ndiyo zinaletwa kwa size mbalimbali, kuna ndogo, medium, large na extra-large. Sasa kuna mtu yeye ni size yake ni small amepewa extra-large, kunahaja gani ya kulalamika, si kurudisha tu ili aweze kupewa kwa size yake. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa, ndugu zangu Kambi ya Upinzani, msiyachukue maneno haya kijumlajumla, haya ni maneno yenye lengo la kugombanisha, nadhani si sawa sisi tukayabeba kwa ujumla namna hiyo. Mimi sioni tatizo lolote, kamasize zipo kuanzia small mpaka extra-large, kwa nini usipate size yako, kama umepewa siyo, ni kiasi cha kubadilisha tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maboresho ya Sheria ya Ulinzi wa Taifa; Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa inaendelea kufanya majadiliano ya ndani yenye lengo la kuboresha Sera ya Ulinzi na kama tulivyosema siku za nyuma, hatimaye tumepata mapendekezo au tuseme maoni ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na vilevile baada ya kupitiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na wenyewe wametoa maoni yao, kazi inayofanyika sasa hivi ni kutayarisha rasmu ya kwenda kwenye Balaza la Mawaziri ili hatiye hii sera iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya ulinzi na usalama kwenye mipaka yetu ya nchi; Wizara inasema zoezi la kurejesha alama za mipaka kimataifa linahitaji fedha na utayari wa nchi husika. Hapa hoja ilikuwa ni kwamba mipaka hakuna alama na kwamba Wizara husika hazijashughulikia tatizo la mipaka kwa maana ya beacons na kadhalika. Mheshimiwa Masoud hili suala amekuwa akilizungumza kila mwaka, lakini tushukuru tu na niseme kwamba hatua zimeanza kuchukuliwa na katika mpaka wetu wa Kenya kazi hii imefanyika, katika mpaka wetu wa Uganda, kazi hii imefanyika na katika mpaka wetu wa Burundi kazi hii imefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipaka mingine tutaendelea kwa kadri fedha zinavyopatikana na mtambue tu, kwamba kazi hii ni kazi ya Wizara nyingi, Wizara ya Ardhi, Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Ulinzi na kadhalika. Kwa hiyo, ni vyema tushukuru kwamba hatua zimeanza kuchukuliwa na tumeanza sasa kuboresha mipaka yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maeneo ya wananchi yaliyochukuliwa na Jeshi Serikali kushindwa kulipa fidia; hii imekuwa ni hoja kwa siku nyingi sana, na naomba nieleze kidogo kuhusu hoja hii kwamba Serikali inatambua umuhimu wa kuhakikisha kwamba wananchi wote wanalipwa fidia kwa kadri uwezo unavyopatikana. Mwaka huu tunaomaliza, tulitenga bajeti ya shilingi bilioni 20.9 kwa ajili ya kulipa fidia katika maeneo mbalimbali. Tumeshafanikiwa kulipa eneo moja la Kilwa, lakini tumeanza kulipa Kakonko kule, na tumeanza vilevile kulipa maeneo kadhaa.

Kwa hiyo, ninachoweza kusema hapani kwamba, sasa hivi Wizara ya Fedha imeshaweka/imeshatenga shilingi bilioni 16 ili tuendelee kulipa maeneo mengine yaliyobaki. Tathmini, uhakiki ulishafanyika katika katika baadhi ya maeneo, samahani, tathmini ilishafanyika, lakini uhakiki ndiyo unaoendelea sasa. Kwa hiyo, kuna eneo la Ilemela kule, maeneo mawili katika Wilaya ile, lakini vilevile kuna maeneo ya Tarime, kuna maeneo ya Makoko, kuna maeneo kadhaa ambayo yanafanyiwa uhakiki, ili fedha zile zianze kulipwa kwa wahusika.

Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge, tuvute subira wakati mchakato huu wa uhakiki wa fedha zilizofanyiwa uthamini unaendelea ili tuweze kukamisha ulipaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi baina ya wananchi na Jeshi, kama vile kubomolewa nyumba, kukatwa mazao ya wananchi na kadhalika; yamezungumzwa sana humu ndani, lakini mimi napenda niseme mambo mawili; kwanza tutambue kwamba maeneo ya jeshi ni maeneo ambayo wananchi wakiambiwa wasikae karibu ni kwa maslahi yao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ningekuwa nayasema haya bila ya matukio yaliyotokea siku za nyuma, pengine ningeonekana nasema tu, lakini tuna mifano hai, yalitokea pale Gongo la Mboto, yalitokea pale Mbagala, kwa nini wananchi waendelee kukaa katika maeneo haya.

Sasa watu tunatofautiana, kuna watu unaweza ukawaambia mnatakiwa kuhama wakahama, kuna watu wengine hawaelewi lugha hiyo, kwa hiyo, lazima hatua zichukuliwe, na ndiyo maama hatua zinapochukuliwa, basi tusiwe tunapiga kelele ni kwa sababu ya maslahi yao wenyewe, haya maeneo mengine ni hatari kwa watu kukaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikubwa zaidi ni kuangalia nani mwenye haki, unapokuwa umevamia katika eneo la Jeshi lililopimwa, lenye mipaka. Kuna njia gani zaidi ya kuzungumza zaidi ya kumwambia mtu atake asitake lazima aondoke, kwa hiyo, ndicho kinachofanyika. Kwa hiyo, sioni kama hili suala tulichukulie kisiasa, tulichukulie kwamba watu wameonewa, watu hawajaonewa, na mpaka haya yametokea, wameshapewa warning mara kadhaa, kila aina ya juhudi zinafanyika na nimwambie tu ndugu yangu aliyezungumia suala hili la kukatwa hii mipapai, ni kwamba Serikali za Mitaa ile, za Vijiji vile, zilitumika kuwashawishi, kuwaambia wananchi wahame, lakini baada ya mbinu zote kushindikana, basi lazima tutumie njia hizi, hakuna njia nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushiriki wa amani nje ya nchi, Waheshimiwa Wabunge kwenye upande wa Upinzani walitaka kujua idadi ya wanajeshi waliopoteza maisha na vilevile na stahili wanazopaswa kupewa endapo wanapoteza maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanajeshi anapoumia au kufariki akiwa katika ulinzi wa amani huwa anapewa malipo ya sehemu mbili, sehemu ya kwanza anapata malipo ambayo yanatiolewa na Umoja wa Mataifa na sehemu ya pili hutolewa na Seikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuzingatia kanuni zilizowekwa za pensheni kwa Majeshi ya Ulinzi.

Kwa hiyo, hakuna utata katika mafao ya wanaopoteza masiha wakiwa katika ulinzi wa amani, fedha hizo zinatolewa kwa pande zote mbili na niseme tu malipo yanayotolewa na Umoja wa Mataifa ni dola za kimarekani 70,000 na fedha za rambirambi ambazo hutolewa na Mkuu wa Majeshi ikiwa ni mishahara ya miezi sita na familia zinasafirishwa pamoja na mizigo kwenda nyumbani. Kwa hiyo, hakuna utata kabisa katika eneo hili na mara zote yanapotokea maafa ya kupoteza watu katika maeneo hayo, Serikali imekuwa ikitoa taarifa na taarifa ziko wazi za idadi ambao wamepoteza maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili nizungumzia pia wajane wa wanajeshi waliofariki, hoja ilikuwa ni kwamba hawatunzwi, ni kwamba wajane wa hawa waopoteza maisha, Serikali imekuwa ikihakikisha kuwa wanatunzwa, wajane na mayatima na kuwapa stahiki zao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi ya jeshi katika kupambana na matukio ya kigaidi nchini; Kitengo cha Usalama na Utambuzi (Military Intelligence) kitumike kusaidia Jeshi la Polisi kubaini na kukabiliana na vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na watu wasiojulikana, mfano kutekwa kwa watu ambao wamewataja. Sasa niseme tu, ni Kambi hii hii ya Upinzani katika hoja yao walisema Jeshi lisiingilie kazi za Polisi, halafu Kambi hii hii inasema, military intelligence isaidie Polisi. Sasa tunachoweza kusema hapa ni kwamba vyombo hivi lazima vifanye kazi kwa pamoja. Military Intelligence lazima iasaidie jeshi la polisi katika masuala ya ugaidi, masuala ya uharamia, masuala ya usafirishaji haramu wa watu na kadhalika, hizo kazi lazima zifanywe kwa pamoja, kwa hiyo, msione kwamba jeshi linaingilia kazi wa vyombo vingine, ni wajibu wao kufanya kazi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi ya Jeshi la Kujenga Taifa katika kuongeza uchumi wa viwanda nchini. Hili linatambulika, Jeshi la Kujenga Taifa linafanya kazi ya viwanda, linafanya kazi ya kilimo, ufugaji na kadhalika. Nia na madhumuni ni kwamba tuhakikishe wanachangia katika ukuaji wa uchumi na wana viwanda kadhaa kama ambavyo nimevitaja katika hotuba yangu vikiwemo Kiwanda cha Mahidi - Ruvuma, Kiwanda cha Kutengenezea Bidhaa za Ngozi - Dar es Salaam, Kiwanda cha Kokoto, Kiwanda cha Kutengeneza Samani - Chang’ombe, Kiwanda cha Maji - Dar es Salaam na kadhalika. Kwa hiyo, viwanda viko vingi, wanaendelea kufungua na biashara mbalimbali, ikiwemo ulinzi na kadhalika, ili tuweze kuchochea uchumi kupitia Jeshi letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ajira Jeshini, wanasema vijana wengi wa JKT kutoajiriwa na Jeshi, nadhani hii niitolee ufafanuzi kidogo. Tunachukua vijana wa kujitolea wengi, kwa mwaka wanaweza wakafika 20,000; hatuwezi kuwaajiri vijana wote hawa, na ieleweke kwamba anayeingia katika Jeshi la Kujenga Taifa, si kwa madhumuni ya kutafuta ajira, ni kwa madhumuni ya kupata stadi za kazi, ni kwa madhumuni ya kupewa stadi za ulinzi wa nchi yake, na hili ni Jeshi la Akiba. Kwa hiyo, hawa huwa wanapewa mafunzo yale ya kijeshi, lakini baadaye wanapewa mafunzo ya stadi za kazi. Wanaobahatika kuajiriwa wanaajiriwa na ambao hawabahatiki wanatakiwa wakajiajiri baada ya kupata stadi za kazi hizo.

Kwa hiyo, vijana wengi wamekuwa wakilalamika lakini nataka ieleweke, kwamba ukijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa, siyo kwamba unaingia kwenye ajira, ni kwamba unakuja kuoata mafunzo ya stadi za kazi na ukakamavu za uzalendo, ili hatimaye uweze kuwa jeshi la akiba kwa ajili ya nchi yako. Kuna baadhi ya nchi ni watu wote lazima wapiti huko. Kwa hiyo, ilie hoja ya kwamba mnawafundisha kutumia dhana za kivita halafu hamuwapi ajira, wala siyo hoja, kwa sababu kuna nchi, kwa mfano Israel, kila mtu, lazima apate mafunzo hayo. Madhumini yake ni nini, madhumuni yake ni kwamba hili ni Jeshi la Akiba, wanapohitajika wakati wa vita, lazima watu hawa wawe wana ujuzi wa kutumia silaha ili waweze kuisaidia nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wa saa za kazi jeshini bado unalalaikiwa, Waheshimiwa Wabunge, mimi nadhani tusiingie huku, wanajeshi wanatakiwa wawe kazini, wawe tayari masaa 24, jeshini hakuna suala la saa za kazi, saa 24 uwe tayari. Ukiwa una mapumziko ni kutokna na kitengo ambacho upo au maeneo ya kazi ambayo unafanya au una majukumu maalum, lakini kwa mara zote inatakiwa masaa 24 watu wawe kazini. Kwa hiyo, hili suala la kulalamikiwa kwa masaa 12, mimi nadhani wala siyo la msingi na tusiingilie kama wanasiasa, tuwaache wenyewe kwa kanuni zao na taratibu zao za kijeshi watekeleze majukumu yao. (Makofi)

Mimi nadhani haitakuwa busara twende na vile mnavyotaka kwamba watu saa tisa wasiwepo, limetokea tatizo, itakuwa sisi wa kwanza kulaumu kwamba Jeshi halikutekeleza wajibu wake, ndiyo maama watu wote wanatakiwa wawe kazini muda wote na tumwachie Mkuu wa Majeshi apange taratibu za kazi kwa wanajeshi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upandeshwaji vyeo kwamba kuna mizengwe, kuna nini, mimi nadhani hizi kauli tujiepushe nazo, hakuna mizengwe, kuna taratibu. Taratibu kupandishwa vyeo JWTZ au tuseme Jeshi kwa ujumla, utaratibu wa kupandisha vyeo maafisa na askari unazingatia mambo yafuatayo; kufanya kazi, kufanya kozi kwa cheo husika, tabia na mwenendo mzuri, utendaji kazi mzuri na kujituma, tabia yake kiusalama, nafasi katika muundo kama ikama ipo, kutimiza muda wa kukaa na cheo kimoja. Sasa haya yote yanafuatwa, asitokee mtu akaja kwa Mbunge akasema kwamba mimi sijapandishwa cheo na kozi nimefanya, kozi siyo kigezo pekee, nimetaja vigezo vingapi hapo, kuna vigezo vingi! (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, tujiepushe na kuchukua maneno haya kutoka kwa vijana hawa au kwa watu ambao hawalitakii mema Jeshi. Mimi nataka nikupeni ushahidi wangu, kwa kipindi nilichokaa katika Wizara hii, watu wamepanda vyeo ninawaona kila wakati. Watu wamepanda vyeo kila wakati kwa sabbu jeshi hili linaendeshwa kwa taratibu na kanuni zinazotakiwa na ndiyo maana tuko vizuri, hata ulinzi wetu uko vizuri, kama ingekuwa kuna matatizo hayo simgeona kuna migomo na vitu kama hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye hoja za Waheshimiwa Wabunge wengine, Mheshimiwa Richard Ndassa alitaka Kambi ya JKT Kanda ya Ziwa, hili limepokelewa litafanyiwa kazi na bila shaka na sisi tunataka hilo litokee. (Makofi)

Mheshimiwa Fakharia alitaka nyumba za wanajeshi ziboreshwe, ni kweli, tunatambua kwamba tuna changamoto ya kuchoka kwa nyumba nyingi za Jeshini, na ndiyo maana tukawa tuna ule mradi wa nyumba mpya. Nyumba mpya zile zimejengwa zaidi ya 6,000, hazitoshelezi, nyumba za zamani kuna bajeti ndogo Wizarani, kuna bajeti ndogo Ngome kwa ajili ya kukarabati nyumba zile, lakini kwa sababu ya upungufu wa bajeti, hatuwezi kufika kote zikawa nzuri kwa wakati mmoja. Tunaomba tuvumilie wakati utaratibu unaendelea awamu kwa awamu kuboresha nyumba na ukarabati wa nyumba za wananchi.

Kuhusu suala la fidia kwa wanaodai, hili nimeshalizungumza, fidia za ardhi, suala la ajira, lini watapata ajira kama alivyosema Mheshimiwa Rais, tunalifanyia kazi liko katika mchakato wa kupanga wale ambao Mheshimiwa Rais alisema wapatiwe ajira, watapata ajira hizo kama ilivyoagizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haki za wastaafu kusumbuliwa, hili Mheshimiwa Fakharia naweza nikasema kwamba tumelipokea, tunaona ugumu wa mtu ambaye amestaafu hajapata mafao kwenda Makao Mkuu kila mara kunaweza kukamgharimu sana. Tutatafuta utaratibu mzuri zaidi wa documents zote kuwekwa sehemu moja pale Zanzibar ili wazijaze na baadae baada ya kukamilisha mchakato huo zipelekwe Makau Makuu ndipo muhusika atakiwe kwenda kule ili kumalizia mchakato.

Mheshimiwa Anatropia alizungumzia bima ya afya, na sisi tunakubaliana kwamba ni muhimu tupate bima ya afya kwa wanajeshi na mchakato wa kuanzisha bima ya afya kwa wanajeshi unaendelea. Sisi kama Wizara tunataka bima ya afya ya wanajeshi itayoendeshwa na wanajeshi na hili tunasababu ya kutaka kufanya hivyo, kwa sababu fedha zitakazopatikana tutaweza kuboresha vituo vyetu, kujenga vipya na kutumia na hospitali nyingine kutoa huduma. Kwa hiyo watu wasiwe na wasiwasi kwamba labda mna vituo vichache hapana, vituo vingine vitatumika ambavyo siyo vya jeshi tukiwa na bima ya afya.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, SUMA kujiingiza kwenye mikataba mibovu, hili lilishazungumzwa Tanzansino, Cami SUMA, Equator wote hawa tulishatolea ufafanuzi katika bajeti zilizopita, mikataba hii imesitishwa kwa sababu haikuwa mizuri na ni nia ya Serikali kuondoa mikataba yote mibovu na sasa hivi mikataba mingine yote tunayoingia tunahakikika inakwenda vizuri ilituweze kupata masilahi kutokana na mikataba hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ile Kampuni ya URSUS, Mheshimiwa Anatropia nikueleze tu kwamba URSUS haifanyi kazi na SUMA JKT, inafanya kazi na NDC, wanakwenda vizuri matreka tunayaona wanaendelea kama kawaida. URSUS hawapo upande wa SUMA. (Makofi)

Mheshimiwa Maryam Msabaha, kuhusu viatu kwamba havina viwango vinavyotakiwa; nieleze tu kwamba viatu sasa vinanunuliwa nchini humuhumu, SUMA JKT wana kiwanda kidogo cha viatu, lakini kuna kampuni zinazozalisha ndani zinanunuliwa humu ndani. Kwa hiyo siyo kweli kwamba tunaendelea kununua kutoka China vyenye kiwango kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uhakiki wa mipaka nilishalitolea maelezo Mheshimiwa Rehani anataka mafunzo ya JKT yawajenge vijana kujitegemea, hili ndiyo tunalolifanya, tunawafundisha stadi za kazi ili waweze kujitegemea na kuna programu chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ya uwezeshaji. Ni matumaini yetu kwamba tukiziunganisha hizi baada ya kupata stadi za kazi na kuwezeshwa vijana hawa wataweza kujitegemea wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, JKT lijitegemee kwa chakula ndiyo nia yetu, ni kweli tunayo maeneo makubwa ya kilimo na ufugaji, tunataka tuwawezeshe JKT kifedha kwa maana kibajeti ili waweze kulima, waweze kufuga wajitegemee wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Ras Mshindo kwamba ijengwe karakana na bandari ya uvuvi, hilo liko katika nia yetu kuweza kuweka karakana pale nzuri kwa ajili ya meli za kijeshi na meli za kiraia, vilevile ikiwezekana kuweka bandari ya uvuvi ili kuweza kupata kipato kwa ajili ya kuendesha Jeshi na Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Malembeka Serikali iangalie jinsi ya kuajiri vijana wa JKT, hili nilishalitolea ufafanuzi Waheshimiwa Wabunge vijana hawa ni wengi, hatuwezi kuwachukua wote, lakini vyombo vyote vya ulinzi na usalama vimetakiwa kuchukua kutoka JKT. Kwa hiyo, baada ya kuchukuliwa na vyombo vyote vya ulinzi na usalama bado wanabaki wengi ni lazima watafutiwe njia nyingine za kujiajiri.Kwa hiyo wasitegemee kwamba wote watapata ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama.

Kuhusu Waziri atoe taarifa ya kupigwa watu kule Afrika ya Kusini, hili lilishatolewa ufafanuzi na Waziri wa Mambo ya Nje kwamba atalitolea maelezo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Jeshi Welezo kwamba haliendani na mandhari ya pale na vitu vinavyofanyika siyo vizuri, hili limeshazingatiwa na limefanyiwa kazi kwa kweli yale mambo ambayo yalikuwa yanaharibu taswira pale yameshaondolewa.

Mheshimiwa Kanali Masoud, Serikali iongeze pensheni kwa wastaafu; hili liko katika mkakati kama nilivyosema awamu kwa awamu, mipaka fedha nyingi za upimaji na fidia hazitoshi Serikali iongeze, tunakubaliana na kadri bajeti itavyoruhusu tutaendelea kupima ili kuondoa migogoro ambayo kila mara inajitokeza. Kuhusu Nyumbu na Mzinga yaboreshwe, nimeshatoa ufafanuzi kwamba wana mipango mikakati sasa ili kuweza kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Salim Jeshi limetumika kiutemi kufyeka mipaka nilishalisemea. Wanajeshi hawalipwi overtime, hakuna Jeshi duniani wanaolipwa overtime, Jeshi dunia nzima wanafanya kazi muda wote. Kwahiyo hakuna suala la overtime jeshini, wanakatwa kodi kwenye mishahara ndivyo utaraibu, Serikali inajiendesha kwa kodi za watu wote, hakuna upendeleo katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mishahara haina tofauti na watumishi umma, hii siyo kweli wana viwango vyao ni tofauti, hawana bima za afya ndiyo kama tulivyozungumza kuhusu bima ya afya na fedha zitumike kwenyepiece keeping ili kupata fedha. Piece keeping tunafanya na hizo re- embracement tunazipata, na tunaweza kuboresha Jeshi kupitia re-embracement hizo.

Mheshimiwa Musukuma ametaka Wabunge wapate mafunzo pale NDC, ni wazo zuri na mimi ninashauri kwa kila mwenye nafasi na atakayependa anaweza ku-apply pale NDC aweze kupata mafunzo kwa kweli itabadilisha taswira au uelewa wa ulinzi katika nchi yetu.

SUMA JKT wapewe ulinzi wa migodi watafanya kazi ya kwenda kushawishi migodi iwape kazi kwa sababu ni uwamuzi wao kumpa wanaemtaka lakini SUMA JKT watafanya kazi hii. Kuhusu bima ya afya, Mheshimwa Mlinga tulishaitolea ufafanuzi, Mheshimiwa Getere alitaka matreka ya SUMA JKT pale kilimo kwanza yaondolewe au wakulima warudishie, hili limepokelewa na Mkuu wa JKT atalifanyia kazi ili kuhakikisha kwamba tatizo hilo linaondoka kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo hoja nyingine kuhusu maeneo mengi ya Jeshi kuvamiwa na wananchi kuanzia sasa au tumeshatoa utaratibu wa kwanza kupima maeneo ya Jeshi ili kuweka mipaka. Nadhani hii ndiyo itaondoa tatizo lote, kwa miaka mingi Jeshi lilikuwa lina maeneo ambayo hayajapimwa hiyo ilitoa nafasi kwa watu kuyavamia, lakini sasa yatapimwa na yatapewa hati miliki, ili kuondoa utata huu wa kuvamiwa mara kwa mara na kuleta migogoro.

Vilevile tutaweka mapango kwa sasa wakati utaratibu huo wa kutafuta fedha za kupima na kupata hati miliki mapango yatawekwa, miti itapandwa ili kuondoa utata wa mipaka ilipo na wananchi waache kuyavamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakuu wa Vikosi wamepewa maelekezo ya kufanya doria mara kwa mara ii watu wasiachiwe wanajenga wanamaliza halafu ndiyo wanakuja kubomolewa, hii iwe inafanyika pale wanapoanza ili kuondoa malalamiko yanayotokana na watu ambao wameshajenga au wameshawekeza vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fedha za mikataba kwamba Serikali itenge fedha za kutosha katika fungu la maendeleo ili kulipa madeni ya mikataba. Hii imekuwa ikifanyika awamu kwa awamu, fedha zote karibu zote ambazo zinawekwa katika bajeti yetu ya maendeleo madhumuni yake ni hayo kulipa mikataba ambayo tumeingia, si rahisi kuilipa yote kwa kipindi kimoja na ndiyo maana kila mwaka tumekuwa tunafanya hivo awamu kwa awamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Mzinga na Nyumbu, nilishatolea ufafanuzi kwamba mashirika haya yana mipango mikakati ili yawezeshwe na yakiwezeshwa yatafanya kazi nzuri zaidi kuliko ambavyo inafanyika sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fedha za chakula kwa wanajeshi kwamba Serikali itenge fedha za kula za kutosha na ziongezwe kiwango, hii hoja imepokelewa, tunaendelea mazungumzo na Hazina ili kuona uwezekano, bila shaka hili linategemea na mapato ya Serikali, lakini kila mapato yakiongezeka na uwezekano ukipatikana kwa sababu tumetoka mbali, hatukuanzana hii fedha ambayo inatolewa sasa hivi tulianza shilingi 3,000 ikaja shilingi 5,000, ikaja shilingi 8,000 sasa shilingi 10,000. Kwa hiyo, bila shaka Serikali itaendelea kuboresha hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sera ya Ulinzi ya Taifa, nimeshalitolea maelezo kwamba mchakato wake sasa umefika hatua nzuri sana na muda si mrefu tutafikisha katika mamlaka husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Serikali itenge fedha kwa ajili ya shughuli za Jeshi ikiwemo barabara, vikosini na barabara za mipakani; kwa kweli mpaka sasa hivi hakuna sera maalum ya barabara za mipakani na fedha hizo haziji katika Wizara ya Ulinzi, fedha hizo bado zinapelekwa Halmashauri, ni wajibu wa halmashauri kuhakikisha kwamba wanaziboresha barabara hizo.

Waheshimiwa wengi walichangia kuhusu vijana wa JKT kuwezeshwa ili waweze kujiajiri. Niseme tu kwamba JKT linaendelea kutoa mafunzo ya stadi za kazi kwa vijana wakujitolea, kupitia shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na kilimo, ufugaji na ufundi. Aidha, kupitia mashamba darasa yaliyopo makambini vijana wanajifunza utaalam mbalimbali wa kilimo na ufugaji utakaopelekea kuwezakujitegemea mara wanapomaliza mkataba.

Vilevile JKT iliingia mkata na Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ikilenga kuwafundisha elimu ya ujasiliamali wakufunzi wanaotoa mafunzo kwa vijana wa JKT; mafunzo hayo yameongeza uwezo vijana kupata elimu iliyoboresha ya stadi za kazi na ujasiriamali. Pamoja na hatua hizo JKT ipo katika mpango wa kujenga Vocational Training Center, Kongwa, Dodoma ili kuweza kuongeza uwezo wa mafunzo ya stadi za kazi kwa vijana ili waweze kujiajiri wenyewe baada ya kuhitimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani mkazo tuweke hapa kwamba hawa vijana wawezeshwe baada ya kupata stadi za kazi wajiajiri kwa sababu si kweli kwamba wote wanaweza kuajiriwa na Jeshi na sasa hivi imekuwa malalamiko mengi, lakini ni kutojua pale wanapojiunga kwamba si wote watakaopata ajira na bila shaka wakiwezeshwa kimafunzo wataweza kujitegemea wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo kero ambazo zilielezwa hapa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kuhusu kumbi za burudani katika Kambi za Jeshi kutumiwa na wananchi badala ya wanajeshi na kuwa chanzo cha ugomvi kati ya wanajeshi na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tueleze tu kwamba mwanajeshi anapokuwa nje ya kazi akifanya makosa anashtakiwa kwa mujibu wa sheria bila kujali kwamba yeye ni mwanajeshi. Kwa hiyo isichukuliwe kwamba kwa kuwa ni mwanajeshi basi anaweza akavunja sheria anavyotaka hilo halipo na tunaweza kueleza hapa kwamba mara nyingi yakitokea matatizo kama haya hata Jeshi lenyewe linachukua sheria, linachukua taratibu za kinidhamu dhidi yao na bila shaka taarifa zikitolewa basi utaratibu wa kisheria na kikanuni utachukuliwa dhidi ya wanaovunja maadili ya kijeshi wanapokuwa nje ya maeneo ya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mbunge alitaka wanajeshi kwamba walipwe mishahara maalum; jibu ni kwamba wanajeshi wote wanapoandikishwa kwa ajili ya ulinzi wa Taifa hulipwa mishahara maaum yaani specific salary na Serikali kila mwezi kwa kuzingatia cheo na muda wa kukaa na cheo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani mengi nitakuwa nimeyatolea maelezo ya ujumla na yale ambayo sijayatolea maelezo moja moja basi kama kawaida yetu tutayapanga ili Waheshimiwa Wabunge waweze kupata maelezo ya maandishi kwa kila hoja ili waweze kujiridhisha na majibu yetu kwa wale ambao pengine majibu yao maswali yao nitakuwa sijaweza kuyatolea ufafanuzi wa kina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami naomba nianze kuchangia hoja hii kwa kuishukuru Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa mimi pamoja na watendaji wangu. Nataka niwahakikishie kwamba tutaendelea kushirikiana nao. Aidha, nawapongeza kwa kazi nzuri wanayoifanya. Tumekuwa tukifanya kazi pamoja nao tukitembelea maeneo mbalimbali na tunawashukuru sana kwa usimamizi wao na ushauri wao kwa Wizara yangu. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja kadhaa ambazo zimetolewa na napenda nianze na zile za Kamati kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la beacons kutokuwepo katika mipaka yetu. Ni kweli hili ni tatizo la muda mrefu lakini napenda niseme kwamba hatua zimeanza kuchukuliwa. Tumechukua hatua za aina mbili. Kwanza ni mazungumzo kati ya Wizara zinazohusika kwa upande wetu wa Tanzania pamoja na ule upande wa majirani zetu. Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii imekamilika kwa mpaka wa Tanzania na Kenya na beacons zimeanza kurudishiwa na mazungumzo yapo katika hatua nzuri kwa upande wa Tanzania na Uganda. Ni mategemeo yetu kwamba baada ya kukamilika kwa mazungumzo hayo, basi tutarusha zile beacons na kuweka buffer zone ili wananchi wasiingilie ile mipaka kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pia imeeleza juu ya suala la marekebisho ya Sheria ya JKT ili iweze kutoa fidia kwa vijana wanaoumia wakiwa kwenye mafunzo. Hili tunalikubali, ni ushauri mzuri sana na ni kweli kwamba wapo vijana wanaopata matatizo ya kiafya na wengine wanaoumia kupitia yale mazoezi yanayofanyika kule. Kwa hiyo, ni jambo ambalo na sisi tunalipokea na tutafanya utaratibu wa kufanya marekebisho ili waweze kupata fidia iwapo watakuwa wameumia wakiwa katika mafunzo. Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja ya idadi ya vijana wa JKT waliochukuliwa mwaka huu. Napenda nitoe taarifa kwamba vijana waliochukuliwa kwenda JKT ni wa aina mbili; wale wa mujibu wa sheria ambao mwaka huu idadi yao ni 14,748 na wale wanaojitolea wamechukuliwa 9,848. Kwa hivyo, hao ndiyo ambao wamepata nafasi safari hii. Tunatambua kwamba idadi hii ni ndogo na inabidi tuwachukue wengi zaidi hususani wale wa mujibu wa sheria na tutaendelea kujenga miundombinu katika makambi yetu ili tuweze kuwa na uwezo mkubwa zaidi wa kuweza kuwachukua walio wengi zaidi. Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hoja hizo za Kamati sasa niingie kwenye hoja za Waheshimiwa Wabunge mmoja mmoja na nianze na ile ya Mheshimiwa Rweikiza ambaye ametaka kujua ni kwa nini hatujasaini na ku-ratify ule Mkataba wa Biological Weapon Convention. Nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Rweikiza kwamba kuna mikataba ya aina hii miwili; wa kwanza ni ule Chemical Weapons Convention na wa pili ni Biological Weapons Convention. Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Chemical Weapons Convention tulishasaini na tumeshauridhia, kwa hiyo, pale tumemaliza. Kwa upande wa Biological Weapons Convention kusaini tulishasaini kilichobaki ni kuridhia na ku-domesticate kwa maana ya kwamba kuingiza katika sheria za nchi ili uweze kutumika katika sheria za nchi. Kazi hiyo inaendelea na iko katika hatua ya Cabinet Secretariat ili hatimaye iweze kufika Bungeni. Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mattar alitoa mapendekezo kwamba asilimia ya vijana wanaochukuliwa kuingia JKT kutoka Zanzibar basi angalau ipatikane asilimia kumi ya wale wa jumla wanaochukuliwa. Tunaweza kusema kwamba kwa sasa hivi au kwa mwaka huu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilipewa nafasi 300 na tunaona umuhimu wa kuongeza nafasi hizo. Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuahidi kwamba mwaka hadi mwaka tutaendelea kuwa tunaongeza idadi hii japo siyo kwa kufikia asilimia kumi ili tuweze kupata vijana wengi zaidi kutoka upande wa pili wa Jamhuri yetu, lakini wakati huo huo lazima tujenge miundombinu zaidi ili tuweze kupata idadi kubwa zaidi ya vijana wanaoingia katika Jeshi la Kujenga Taifa. Mheshimiwa Mwenyekiti, naye vilevile alishauri kwamba badala ya utaratibu unaotumika sasa ule wa kupitia Wilayani na Mikoani alishauri kwamba pengine vijana wachukuliwe kutoka JKU. Ambacho naweza kumwambia Mheshimiwa Mbunge kuhusu hili ni kwamba uamuzi wa jambo hili upo juu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi yetu sisi au mimi kama Waziri wa Ulinzi huwa napeleka nafasi zile kwa Makamu wa Pili wa Rais na tunawaachia jukumu la kuamua wao wanataka kutumia utaratibu gani. Mpaka sasa wamekuwa wakizigawa Wilayani na Mikoani. Kwa hivyo, naweza kumshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba ni vyema akazungumza na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuangalia utaratibu kama huo wa JKU utakuwa ni bora zaidi. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya Mheshimiwa Zitto Kabwe ya kuhusu Kanali Kashmir kwamba hajastaafishwa rasmi. Kwanza nataka nimpe taarifa ya kwamba Kanali Kashmir ni kweli alikuwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na cheo chake kilikuwa ni Chief of Logistics and Engineering (CLE) na sio Chief of Staff. Chief of Staff wakati wake yeye cheo hicho hakikuwepo ni baada ya yeye kutoka mwaka 1974 ndipo kilipoanzishwa cheo cha Chief of Staff. Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni kwamba kuhusu maslahi ya kustaafu ni suala la kisheria. Kama ni kweli kuna uthibitisho kwamba Kanali Kashmir hajalipwa jambo hili litaangaliwa kisheria aweze kupata mafao yake. Hata hivyo, taarifa nilizokuwa nazo ni kwamba wakati anatoka Jeshini kwenda SUDECO fedha za Jeshi alikuwa ameshapata na baada ya kustaafu kule SUDECO alitakiwa alipwe upande ule ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mengine nitayaleta kwa maandishi. Naunga mkono hoja na ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nichangie hoja na hususani nitajikita katika Kamati ya Mambo ya Nje ya Ulinzi na Usalama. Kwanza niipongeze Kamati kwa kazi nzuri wanayoifanya na niwashukuru kwa ushirikiano wanaotupa mimi pamoja na watendaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja zilizotolewa ya kwanza ni kukosekana kwa Sera ya Ulinzi wa Taifa nchini na kuna athiri ufanisi katika utendaji. Tunakiri mpaka sasa hivi sera hiyo haijapatikana lakini nataka niseme kwamba sera hiyo tayari rasimu yake ipo imekwama katika jambo moja dogo nalo ni maoni ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni nilipata nafasi ya kuzungumza na Waziri mhusika kule Zanzibar akaniambia kwamba tayari wanajipanga kwenda kuijadili katika Baraza la Mapinduzi ili hatimaye waweze kutufikishia maoni yao na baada hapo itafuata utaratibu uliobaki ili tuwe tuna sera ya ulinzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimshukuru Mheshimiwa Angelina Mabula kwa kulijibu lile suala la beacons za mipakani kama mlivyosikia kazi imeanza kufanywa na vilevile nimpongeze Mheshimiwa Kandege kwa kujibu hoja za barabara za mipakani jambo hilo litashughulikiwa na TAMISEMI na tuna imani kwamba barabara hizo zitapitika ili ulinzi uweze kufanyika vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu madeni ya Shirika la SUMA JKT, ni kweli kuna madeni mengi kuna madeni ya matreka, kuna madeni ya huduma zinazotolewa na SUMA Guard ya ulinzi kuna madeni ya mbegu zinazozalishwa na SUMA na kuuzwa katika taasisi mbalimbali. Lakini hatua zimeanza kuchukuliwa za kukusanya madeni hayo tulikuwa tunawa andikia barua lakini sasa hivi tume-engage kampuni za ukusanyaji wa madeni ili hatua stahili ziweze kuchukuliwa na fedha hizo zipatikane ili SUMA ijiendeshe vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wananchi kutolipwa fidia katika maeneo yaliyotwaliwa wanajeshi na migogoro ya ardhi kwa ujumla, nataka hapa niseme Waheshimiwa Wabunge ipo dhana kwamba Jeshi lina maeneo makubwa ambayo hayatumiki. Nataka nisemie hivi kwamba jeshi lina maeneo makubwa kweli lakini yalichukuliwa kwa sababu maalum. Yako maeneo ya Jeshi kambi za Jeshi ambazo kazi zake ni utawala na logistic, lakini kuna kambi za mapigano, kuna vifaa vya milipuko, kuna kambi za mapigano, kuna vifaa vya milipuko, kuna kufanya mazoezi ni lazima wawe na maeneo makubwa.

Kwa hiyo, ninachosema hapa ni kwamba watu wasidhani kwamba kuna mapori wakadhani hayahitajiki wakavamia hiyo sio sahihi kwa sababu pale wanafanya mazoezi. Kambi zote lazima zifanye mazoezi, kwa maana hiyo ni kwamba maeneo makubwa yanahitajika jeshini na wananchi waelewe hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa wale wananchi waliovamia tungewataka na pamoja na nyinyi Waheshimiwa Wabunge niwaombe kwamba isiwe kawaida ya Wabunge kutetea upande wa wananchi peke yake, kwanza tuangalie tuhakikishe kwamba wananchi wana haki. Yako maeneo mengi wananchi ndio wamevamia maeneo ya jeshi, na ninyi mnatambua, kila kwenye Kambi ya Jeshi kwa sababu kuna huduma kuna afya pale, kuna shule pale, kuna maji pale wananchi wanakuwa haraka kuja karibu na wengine huwa wanalima katika maeneo yale. Kwa hiyo, tunaomba kwa sasa tuhakikishe kwamba wale wananchi ambao hawana haki ya kuwa katika maeneo hayo waondolewe na ndugu zangu mtusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa wale wanaodai fidia, kweli kuna maeneo ambayo Jeshi limetwaa tutahakikisha kwamba wanalipwa na haki zao watazipata na kwa kadri ya uwezo wa kifedha tutaendelea kulishughulikia suala hili ili wananchi wale waweze kupata haki zao.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nichangie kwenye hoja iliyo mbele yetu kwa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. Naipongeza Kamati, nawashukuru sana kwa ushirikiano wanaotupa mimi pamoja na watendaji wa Wizara yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye maoni na mapendekezo ya Kamati juu ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Kulikuwa kuna hoja ya kukosekana kwa Sera ya Ulinzi wa Taifa nchini ambayo inaathiri ufanisi katika uratibu wa ulinzi wa Taifa, napenda niliarifu Bunge lako kwamba tatizo hili sasa limekwisha. Kwa muda mrefu tulikuwa hatuna hii sera kwa sababu hakukuwa na maoni ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Napenda niliarifu Bunge lako kwamba maoni hayo sasa yamepatikana, mchakato unaendelea ndani ya Wizara ili kuikamilisha sera hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kukosekana kwa alama za mipaka ya nchi (beacons) kunachangia uvamizi wa raia wa kigeni katika baadhi ya maeneo ya mipaka, jambo ambalo linaweza kuathiri ulinzi na usalama wa nchi. Nataka niwaeleze Waheshimiwa Wabunge kwamba na eneo hili nalo limeanza kufanyiwa kazi kwa nguvu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mipaka yetu upande wa Kenya na upande wa Uganda tayari beacons zimeanza kurudishiwa, upande wa Kenya tayari tuna kilometa zipatazo 172 kati ya 760 ambazo tayari wameshaudishia beacons kuanzia kwenye Ukanda wa Ziwa Victoria kuelekeza Ziwa Natron. Kwa hiyo zoezi hili linaendelea na tumeanza upande wa Kenya na Uganda, tutaendelea katika maeneo mengine, lakini nia na madhumuni ni kurudisha beacons hizo ili kuwepo na uhakika wa kwamba mipaka kati yetu na nchi jirani inajulikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, madeni kwa mashirika yaliyo chini ya SUMA JKT yanaathiri shughuli za uzalishaji mali wa shirika; tunakubali kwamba Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT) lina madeni mengi hususan ule mrdai wao wa matrekta. Nataka nitoe taarifa hapa kwamba toka Mheshimiwa Rais ametoa agizo la wale wote wanaodaiwa waweze kurudisha fedha zile, shirika limeweza kukusanya Sh. 2,900,000,000 na tunaendelea na mchakato huo na baada ya hapo kuna Kampuni maalum ya SUMA JKT ya auction ambayo itachukua hatua za kisheria dhidi ya wale wote ambao watakuwa wameshindwa kulipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukosekana kwa uzio katika baadhi ya Kambi za Jeshi kunasababisha migogoro ya ardhi kutokana na wananchi kuvamia maeneo hayo; ni kweli kwamba maeneo mengi ya Jeshi hayana uzio na hayawezi kuwa na uzio kwa sababu ni maeneo makubwa
sana. Tunachokifanya sasa hivi ni kwamba kuna maagizo kwa kila Mkuu wa Kikosi kuhakikisha kwamba wanaweka alama katika borders zao na hususan yale maeneo makubwa sana, wapande miti na waweke mabango yanayoonesha kwamba haya ni maeneo ya Jeshi, nia na madhumuni ni kuhakikisha kwamba wananchi wanaelewa mipaka ilipo na hawaingiliwi katika maeneo hayo. Baadhi ya maeneo hayo ni ya mazoezi, kwa hiyo wananchi wakiingia huko wanaweza kupata athari kubwa kutokana na dhana zinazotumika katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja nyingine kwamba wananchi kutolipwa fidia katika maeneo yaliyotwaliwa kwa ajili ya matumizi ya Jeshi kumeendelea kusababisha migogoro ya ardhi kati ya wananchi na vikosi vya Jeshi. Hapa ni kama nilivyosema, migogoro ya ardhi kati ya wananchi na Jeshi ipo ya aina kadhaa; moja ni pale wananchi wanapovamia maeneo ambayo tuna uhakika ni ya Jeshi kwa sababu ya ufinyu wa ardhi ya kulima na kufuga, hao hakuna hoja, ni kuwaondoa tu kwa sababu lazima Jeshi libaki na maeneo yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yapo maeneo yaliyotwaliwa kweli na wananchi hawa wanastahili fidia, tumeweka katika bajeti ya mwaka huu shilingi bilioni 20 na mpaka sasa hivi tumeshapokea karibu shilingi bilioni 3 ambazo tumeanza na kulipa eneo la Kilwa ambapo tunaweka base ya Navy. Kwa maana hiyo, kila fedha hizi zitakapoendelea kutolewa wananchi hawa wenye stahili za kulipwa fedha kwa sababu walihamishwa katika maeneo yao wataendelea kulipwa ili migogoro hiyo iishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ilikuwa ni uchakavu wa majengo ya Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi cha Monduli kunashusha hadhi ya chuo hicho kinachotoa mafunzo ya kimataifa. Tumekuwa na jitihada mbalimbali za kukiendeleza na kukiboresha chuo kwani ni cha muda mrefu na baadhi ya majengo yake yamechakaa. Nataka nieleze kwa mfano makazi, katika ule mradi wetu wa nyumba 6,064 pale Monduli wamepata nyumba hizo kwa ajili ya Askari na kuna baadhi ya majengo mapya yamejengwa mfano mzuri ni maktaba, kuna maktaba mpya pale lakini tunaendelea kukarabati Ofisi na maeneo mengine kwa awamu kadri bajeti inavyoruhusu. Tunaelewa kwamba chuo hiki sasa ni cha kimataifa kinachukua wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ya SADC na East African Community kwa maana hiyo kuna kila sababu ya kukiboresha ili kiwe na hadhi inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna eneo la kutotolewa kwa fedha za maendeleo kwa Shirika la Nyumbu na Mzinga kumeendelea kuathiri shughuli za kitafiti na ubunifu wa shirika hilo. Ni sahihi kwamba kwa kipindi kirefu Mashirika haya ya Nyumbu na Mzinga yamekuwa hayapati bajeti inayostahili na kwa maana hiyo kazi zao zimeendelea kupungua. Nataka nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba tayari kuna mpango mkakati maalum kwa mashirika yote mawili haya ambayo yana bajeti na mpango huo tunaupeleka Serikalini ili kuhakikisha kwamba fedha hizo zikipatikana basi mashirika haya yanaweza kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja nyingine iliyotolewa ya ubovu wa barabara za mipakani. Hapa nataka nilieleze suala hili kwamba mpaka sasa hivi sera iliyopo haiweki barabara hizi chini ya Wizara ya Ulinzi au Jeshi la Wananchi, barabara hizi bado ziko kwenye mamlaka ya Halmashauri za Wilaya. Ndiyo maana tunapata tatizo kwa sababu zinakuwa siyo za kipaumbele chini yao matokeo yake ni kwamba barabara nyingi hazina hadhi inayotakiwa. Tunaweza kushauri hapo baadaye tutakapokutana kati yetu sisi, TAMISEMI na wenzetu wa Ujenzi kuona kwamba ni muhimu tukatafuta mpango maalumu kwa ajili ya barabara hizi. Hizi ni barabara za kiulinzi zinatakiwa zipitike muda wote kwa sababu huwezi kujua tatizo litatokea lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, tunapokea ushauri wa Kamati, tutakaa na wadau wote ili tuone njia nzuri zaidi. Tukiwezeshwa kibajeti hata Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania wanaweza wakazitengeneza barabara hizi ili ziweze kupita wakati wote pale zitakapohitajika ziweze kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge mmoja alielezea suala la Jeshi kugeuka kuwa la kiuchumi. Nataka nieleze tu kwamba Jeshi lina matawi ya kiuchumi. Suma JKT, Nyumbu na Mzinga ni sehemu za Jeshi na mashirika yote haya yanafanya biashara. Kwa maana hiyo, siyo kwamba wakati huu wa amani Jeshi limekaa tu kuna biashara kubwa zinazofanyika mfano mzuri ni Suma JKT. Suma JKT wana viwanda vingi tu ikiwemo kiwanda cha maji, kiwanda cha ushonaji, kiwanda cha kutengeneza viatu, wako kwenye kilimo na ufugaji na wana miradi mingi mbalimbali. Nia na madhumuni ni wapate fedha ili kutatua matatizo ya Jeshi ambayo yako nje ya bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba na mimi nichukue fursa hii niwataarifu wenzetu wa Kamati kwamba mapendekezo yao tumeyapokea, tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja hii iliyokuwa mbele yetu. Naomba niishukuru Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa maoni waliyotoa juu ya Wizara yangu ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, Kamati ilitoa maoni kwamba kukosekana kwa Sera ya Ulinzi wa Taifa kunaathiri ufanisi. Napenda niwaeleze tu kwamba sasa hivi tuko pazuri sana. Sera hii ilichelewa kwa muda kwa sababu tulikosa maoni ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kipindi kirefu, lakini nafurahi kulijulisha Bunge lako kwamba maoni yameshapatikana kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na kwamba kwa sasa wadau wanashirikishwa kwa maana ya vyombo vyote vya ulinzi na usalama kupitia maoni hayo; na rasimu ya sera yenyewe ili hatimaye ikamilishe mchakato ambao ni kupita katika Baraza la Makatibu Wakuu na hatimaye Baraza la Mawaziri. Nina imani kwamba suala hili litakamilika ili tuweze kupata sera na kazi zetu ziendelee vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, kukosekana kwa beacons za mipakani kunaathiri ulinzi. Ni kweli kwamba katika mipaka yetu kuna wananchi wamekuwa wakitoa beacons zile na kufanya shughuli za kibinadamu katika maeneo ya mipaka. Hili suala limeshughulikiwa kwa maana kwamba Wizara zote zinazohusika na suala hili; Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Wizara ya Ardhi, pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje, tulishakaa tukaamua kwamba sasa wakati muafaka umefika wa kurudisha beacons katika maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vikao vilifanyika na wenzetu wa Kenya, Uganda na nchi nyingine na zoezi limeanza. Kwa upande wa Kenya tumesharudisha baadhi ya beacon na vilevile tunaendelea katika mpaka wa Tanzana na Uganda kurudisha beacon hizi. Kwa hiyo, suala hili linashughulikiwa na kiwango kikubwa kazi imeanza kufanyika.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna suala la madeni ya Suma JKT kwa upande wa matekta. Ni kweli kwamba fedha bado hazijalipwa takribani shilingi bilioni 34, lakini juhudi kubwa zimefanyika na hivi karibuni tumeweza kukusanya zaidi ya shilingi bilioni tatu katika hatua hizo mpya. Tumeingia mikataba mipya na wale wote waliokuwa wamekopa ili sasa tuweze kuwafuatilia kwa karibu. Vilevile tumeweka Kampuni ya Udalali ya Suma JKT ambayo itakuwa inawapitia wote wanaodaiwa kwa madhumuni ya kuwadai na kuweza kurudisha fedha hizo. Kwa hiyo, hatuna shaka kwamba baada ya muda siyo mrefu tutaweza kuwa tunazirudisha fedha hizi ili ziweze kutumika kwa makusudio yaliyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya kutotolewa kwa fedha kwa Shirika la Nyumbu kunaathiri shughuli za utafiti wa shirika hilo. Ni kweli kwamba kwa muda mrefu fedha zinazotolewa kwa nyumba zimekuwa haba, mwaka huu wa fedha tuna shilingi bilioni 2.5 katika bajeti yao ambayo haikidhi kwa kweli. Nyumbu wamekuja na utaratibu mpya wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Kumi wa Shirika ambao wameutengeneza vizuri na wameweka bajeti ambayo kwa kweli itapita Serikalini. Tukiweza kupata fedha hizo shirika litarudi katika utaratibu wake wa awali wa kufanya tafiti za mazao ya kijeshi ili hatimaye tuweze kulirudisha katika ile dhamira ya kuwepo kwa shirika hili la Nyumbu.

Mheshimiwa Spika, ukiacha Kamati ambayo hoja zake zilikuwa ni hizo ambazo nimeshazitolea ufafanuzi, Mheshimiwa Maige alizungumzia kurudisha beacons ambayo na yenyewe nimeshaizungumza na Mheshimiwa Masele alisema Serikali iendelee kuipatia bajeti mashirika ya Nyumbu na Mzinga ili yaendelee kuzalisha mazao ya kijeshi na kudhibiti ulinzi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza, mashirika yote mawili la Nyumbu na lile la Mzinga wameshatengeneza Mipango ya Maendeleo ya Miaka Mitano kwa Nyumbu na Miaka Kumi kwa Mzinga. Kwa maana hiyo, ni kwamba katika mipango ile ya muda mrefu wameweka bajeti zao pia, ni matarajio yetu kwamba bajeti hizo zitapatikana mwaka hadi mwaka katika kipindi hicho ili waweze kutekeleza majukumu yao kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna pongezi kwa Suma JKT kwa kazi nzuri ya ujenzi wanayoifanya katika maeneo mbalimbali kama Mererani, Ofisi za Serikali hapa Dodoma na kutoa mafunzo kwa vijana wetu. Tunapokea pongezi hizi na tunaahidi Bunge lako kwamba Suma JKT wataendelea na kazi zao za msingi za kulea vijana na vilevile kuzalisha mali.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)