Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Khamis Yahya Machano (1 total)

MHE. JAKU HASHIM AYOUB (K.n.y. MHE. KHAMIS YAHYA MACHANO) aliuliza:-

Tarehe 19 Agosti, 2019, zaidi ya wanafunzi 100 walisafiri kwenda masomoni China na India na ni ukweli kuwa elimu ya juu ni suala la Muungano:-

(a) Je katika wanafunzi hao ni wangapi wanatoka Zanzibar pamoja na majina yao?

(b) Je, ule utaratibu wa Zanzibar kupewa Scholarship bado unatekelezwa?

(c) Je, ni lini Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia atakutana na Waziri wa Elimu Zanzibar ili kuweka utaratibu mzuri wa masuala ya elimu ya juu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khamis Yahya Machano, Mbunge wa Chaani lenye vipengele (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi za ufadhili wa masomo kutoka nchi au mashirika rafiki huratibiwa kwa ushirikiano baina ya pande mbili za Muungano. Mara baada ya kupokea nafasi hizo, Wakurugenzi wenye dhamana ya Elimu ya Juu kutoka pande mbili za Muungano hukutana kwa lengo la kubainisha sifa za waombaji. Matangazo kwa waombaji wote hutolewa kupitia tovuti za Wizara husika. Aidha, zipo nafasi za ufadhili wa masomo ambazo huratibiwa na nchi au shirika linalofadhili.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2019/2020 Serikali ya Watu wa China, kupitia Wizara yangu ilitoa nafasi 61 za ufadhili wa masomo. Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, iliratibu zoezi la kuwapata waombaji wenye sifa. Jumla ya waombaji 82 kati ya 662 walioomba walikidhi vigezo na majina yao kuwasilishwa Ubalozi wa China kwa hatua za uchaguzi. Baada ya mchujo uliofanywa na Ubalozi waombaji 61 walipata ufadhili huo.

Kwa upande wa India, nafasi za ufadhili wa masomo kwa mwaka 2019/2020 zilitangazwa na kuratibiwa na Ubalozi wa India ambapo jumla ya Watanzania 24 wamenufaika. Nafasi za ufadhili wa masomo zinapatikana kwa njia ya ushindani kwa kuzingatia sifa na vigezo na pasipo kujali mwombaji anatoka upande upi wa Muungano.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vikao vya Mawaziri, upo muongozo rasmi kuhusu vikao vya pamoja baina ya pande mbili za Muungano na vikao hivyo hufanyika kutokana na uhitaji. Vikao hivyo vipo katika ngazi ya Kamati ya Pamoja, Kikao cha Mawaziri na Kikao cha Makatibu Wakuu.