Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Joseph George Kakunda (62 total)

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Kwa kuwa kulikuwa na maelekezo Serikalini kuhusu ushirikiano wa karibu kati ya Wizara za Kisekta za SMT na zile za SMZ ambayo yalikuwa yanahimiza ushirikiano wa karibu wa kitaalamu na utafiti na pale Wizara ya Maji ilikuwa imepangwa, Waziri wa Sekta ya Maji Bara na Zanzibar tarehe 8 Juni, 2014; mkutano ule ukaahirishwa kusubiri Bunge la Katiba:-
Je, kwa sasa hivi maelewano hayo yanaendeleaje kuimarishwa? Ahsante sana.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya kazi ya Ofisi ya Makamu wa Rais ni kuratibu mahusiano kati ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mambo yasiyo ya Muungano. Mwezi wa kwanza tumetengeneza ratiba ya vile vikao ambavyo viliahirishwa na mambo ambayo yalibaki kufanyika katika kuhakikisha kwamba mahusiano hayo yanaimarishwa.
Kwa hiyo, moja ya kikao kilichopangwa kufanyika na ambacho tumeweka fedha kwenye bajeti ili kifanyike, ni pamoja na hicho unachoongelea Mheshimiwa Mbunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kuwapa faraja na taarifa wenzetu wa Zanzibar kwamba tumedhamiria kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba Muungano wetu unaimarika katika mambo ya Muungano na yale yasiyo ya Muungano na kazi hiyo tutaifanya kwa nguvu ili kutimiza ahadi yetu kama tulivyowaahidi Watanzania. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Matatizo ya maji kwenye maeneo ya Shinyanga na Korogwe ni sawa na matatizo kwenye maeneo yetu. Naomba Serikali ituambie na iwape matumaini wananchi wa Tarafa za Sikonge, Kiwele, Inyonga mpaka Kwilunde ambako yeye Mheshimiwa Kamwelwe anawakilisha; ni lini sasa shida za maji za wananchi hao zitapungua au zitaisha kabisa? Ahsate sana.
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Sikonge, niseme kwamba tulikuwa tumetoa nafasi kwamba kila halmashauri ilete vipaumbele ya vijiji ambavyo wataanza navyo katika kutekeleza programu ya maji. Kwa hiyo, hayo maeneo anayoyasema Mheshimiwa Mbunge naamini kabisa halmashauri yake imeweka ndivyo vipaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema katika miaka mitano tunataka tupeleke miradi ya maji, kwa maana ya upatikanaji wa maji na ule mtawanyiko utakuwa kwa asilimia 85 ikifika mwaka 2020. Katika kutekeleza miradi hii ndiyo wao watachagua ni ipi tuanze na maeneo yale ambayo hayana maji kabisa wangeweka ndiyo kipaumbele ili kusudi tufikie asilimia hii tunayotaka kuifikia tukifika mwaka 2020. Kwa hiyo, yeye ndiye anajua vizuri zaidi majina ya vijiji na zile kata na wao ndiyo wanatakaoweka vipaumbele, Serikali tutaviwekea bajeti ili tuweze kufikia lengo na wananchi wetu waweze kupata maji.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa kuwa matengenezo aliyosema Mheshimiwa Naibu Waziri yalihusu kukwangua tu na kusawazisha barabara, badala ya kuweka kifusi na kushindilia, hali ambayo imesababisha mvua kidogo tu iliyonyesha, tatizo la mashimo kurudi pale pale. Je, ni lini Serikali itatengeneza barabara hiyo, kwa kuweka kifusi na kushindilia ili iwe imara kabla hata ya lami? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye bajeti iliyosomwa jana, imepangiwa shilingi bilioni 120 kujengwa kwa lami kuanzia mwakani, ambayo ni asilimia 17 tu ya mahitaji yote ya fedha yanayohitajika. Pia Mheshimiwa Waziri hajajibu swali langu la mwisho sehemu (c); Je, ni lini barabara hiyo itakamilika kwa kiwango cha lami?
Naibu Spika, wakati mvua inanyesha, suala la kuweka kifusi nadhani lisingekuwa muafaka, kwa sababu ukiweka kifusi kitaharibu zaidi badala ya kujenga. Hivi sasa mvua kwa kuwa imekwisha suala sasa la kuimarisha kikamilifu hiyo barabara litafuatia.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakumbuka kwamba nilishatoa maelekezo kwa Mameneja wote wa Mikoa sasa kuelekeza nguvu zao kufungua barabara zote nchini ambazo zilijifunga.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la pili, namwomba Mheshimiwa Mbunge akiri kwamba hiki kiasi ambacho amepangiwa, kinatosha ukilinganisha na mahitaji makubwa ya Waheshimiwa Wabunge wengi humu ndani.

WAZIRI WA UJENZI UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nami niongezee baada ya majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Barabara hii inafadhiliwa au inajengwa kutokana na pesa za Benki ya Afrika (ADB).
Kwa kawaida, barabara hii tutaigawa kwenye lots mbalimbali kwa sababu ni barabara ndefu sana. Kwa kawaida barabara hii kuanzia mwakani inaweza kuchukua baina ya miaka mitatu mpaka miaka minne, itakuwa imekamilika, itategemea hali ya hewa inavyokwenda.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
La kwanza, kabla ya kuvunjika kwa uhusiano wetu na nchi ya Israel kulikuwa na miradi mingi ya kimaendeleo inatekelezwa, mfano Hospitali ya Bugando, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Soko la Kariakoo na miradi mingine mingi. Je, baada ya sasa kuwa tumerudisha uhusiano hali ya ushirikiano wa miaradi ya maendeleo ikoje?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; kufungua Ubalozi kwenye nchi fulani inahitajika fedha nyingi sana kuendesha. Na ndiyo hali hiyo husababisha nchi kuwa na Balozi chache au nyingi. Sasa kwa sababu, sasa hivi tuna mwendaokasi wa kufungua Balozi mpya, Israel, Kuwait, Qatar na kadhalika. Je, uwezo wetu kama nchi kwa sasa unakidhi kufungua Balozi mpya kwenye nchi nyingi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la kwanza, kwamba kabla ya mahusiano yetu kuvunjika na watu wa Israel tulikuwa na miradi mingi sana ya kimaendeleo na akihusisha mradi wa Bugando na anasema sasa baada ya kufungua hali itakuwa vipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana nimesisitiza nimesema kutokana na kwamba sasa hivi Sera za Kimataifa zimebadilika na Tanzania imeamua kubadilika. Na kwa sababu tunasisitiza Sera ya Diplomasia ya Kiuchumi miradi hiyo ambayo ilikuwa imesimama wakati ule, ndiyo maana tunataka tuanzishe mahusiano haya kwa karibu ili kuweza kuendeleza miradi iliyokuwepo, lakini vilevile kufungua fursa mpya.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika suala la pili ambalo Mheshimiwa Mbunge ana wasiwasi kwamba sasahivi kumekuwa na mazoea au mpango mkakati wa kufungua Balozi nyingi zaidi na ufunguzi wa Balozi unahitaji pesa nyingi. Na mimi nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge, kama nilivyokuwa ninajibu wakati wa Bajeti kwamba Balozi hizi zitafunguliwa kutokana na uwepo wa pesa itakaokuwanao Serikali ya Tanzania. Sisi tunaelewa kwamba, ufunguzi wa Balozi ni gharama, lakini pia, gharama hiyo ya kufungua Balozi moja baada ya nyingine itategemea kwamba tutafaidika vipi katika ufunguzi wa Balozi hizo. Hatutafungua tu Balozi kwa sababu tunataka kufungua, lakini tutaangalia pia kwamba, tuna uwezo kiasi gani, kwa sababu pia ufunguzi wa Balozi unailetea faida Tanzania. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Nina swali dogo tu, nawaunga mkono wanaharakati wote kuhusu suala hili muhimu, sasa nauliza Serikali, je, itakuwa tayari kuingiza kipengele kwenye sheria ambacho kinazuia kuzaa kabla ya kufikisha miaka 18? Maana wapo watoto wanazaa wana miaka 13 au 14, lakini hawachukuliwi hatua yoyote. Je, Serikali itaweka kipengele kuzuia? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni suala lenye utata kidogo na katika hatua hii kwa kweli, hatujalifikiria hilo. Naomba tuchukue wazo lake tulifanyie kazi tuone kama ni jambo ambalo angalau linaweza hata likafikiriwa kwa sababu lina utata sana.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Uvuvi katika bahari na katika maziwa makubwa unafanyika usiku na mchana, lakini uvuvi katika Mto Koga kule Sikonge unafanyika mchana tu usiku Serikali inakataza. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, ni kwa nini Sikonge tu ndiko uvuvi unakatazwa usiku wakati ndiyo kuna samaki wengi? Ahsante sana.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, Sikonge nimekaa miaka mitano kama Mkuu wa Wilaya na kwa hivyo hiki anachokisema nakifahamu vizuri sana. Ni kweli kwamba uvuvi katika mito na mto huo bahati mbaya eneo ambalo uvuvi unafanyika ni ndani ya hifadhi. Kwa hivyo, ili kuzuia shughuli ambazo si za kivuvi wakati wa usiku ndiyo maana imepigwa marufuku kufanya uvuvi usiku katika eneo hilo. Pia katika Mto huo Koga uvuvi pia unafanywa kwa msimu, wakati ule ambako shughuli za uwindaji katika hifadhi hiyo haziruhusiwi na uvuvi pia unazuiwa ili kutoa nafasi kwa samaki kuzaliana kwa ajili ya msimu unaofuata.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri kuhusu masuala ya ajali barabarani. Sasa nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, Tarafa ya Kitunda ambayo iko umbali wa kilometa 180 kutoka Makao Makuu ya Wilaya ya Sikonge ina Kituo cha Polisi kidogo ambacho kina polisi wanne ambao hawatoshi kuhudumia wakazi zaidi ya 80,000 kwenye Tarafa hiyo. Maana kuna majengo chakavu, polisi wenyewe ni wachache na hawana gari hata moja; lini Serikali itawasaidia polisi hao ili wafanye kazi yao vizuri? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mwezi Machi, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Nyahwa alichinjwa kama kuku na hadi leo wauaji wale hawajakamatwa. Ni lini Serikali itafanya kazi yake kikamilifu ili wauaji hao wakamatwe na kuondoa hofu Kijiji cha Nyahwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Kakunda kwamba concern yake ambayo amei-raise hapa tutaifanyia kazi ya kwa maana ya kwamba tutaongeza idadi ya askari katika kituo hicho. Kwa hiyo, nachukua fursa hii kuwaelekeza Jeshi la Polisi wale askari ambao wako depot, tunaotarajia kuwa-deploy karibuni, basi tuangalie uwezekano wa kuwapeleka Sikonge kuongeza ile idadi ya askari waliopungua pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia pale ambapo magari ambayo tunatarajia yataingia wakati wowote, nayo tuone uwezekano wa kufanya hivyo kwa kuzingatia changamoto eneo hilo baada ya kulifanyia utafiti wa kina pamoja na mahitaji ya nchi nzima.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Barabara ya kutoka Mbeya hadi Mkiwa inaunganisha Mikoa mitatu ya Mbeya, Tabora na Singida na iliamuliwa kujengwa miaka 10 iliyopita. Sasa kipande cha kutoka Chunya hadi Itigi kitakamilika lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoingelea Mheshimiwa Mbunge imepangwa katika bajeti ya mwaka huu utakaoanza Julai. Kwa kweli nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wameipitisha bajeti. Hivyo, ni wajibu wetu kuhakikisha bajeti hiyo tunaisimamia ili itekelezwe kama ilivyopangwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kusema ni lini barabara hii itakamilika, namwomba sana Mheshimiwa Mbunge atupe subira kwa sababu hivi vitu ni vya kitaalam, vinatakiwa vifuatane na mikataba ilivyo. Namhakikishia kwamba barabara hii itakamilika – hilo ndilo la msingi. Lini hasa; nadhani tusiende sana kwa undani kiasi hicho ili baadaye tukaja kushikana uongo hapa.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza, wananchi wamekuwa wanalalamika sana kwamba vijiji ambavyo vimeshapatiwa umeme hadi sasa wanaopewa kipaumbele cha kuunganishiwa umeme ni wale tu wanaokaa kandokando ya barabara kuu. Je, ni lini wananchi wote ambao vijiji vyao vimeunganishiwa umeme watapatiwa umeme wanaohitaji?
Swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri aliahirisha mwezi uliopita safari yake ya kuja Sikonge kujionea matatizo. Je, ni lini sasa atapanga ziara yake kuwatembelea wananchi wa Sikonge?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa REA Awamu ya II inayoendelea ambayo itakamilika mwezi huu, mpango wake mahsusi ulikuwa ni kupeleka umeme kwenye vituo vya vijiji na siyo kusambaza kwenye vitongoji. Sambamba na hilo, kabla hatujaanza Mradi wa REA Awamu ya III, kuna mradi mwingine unaosambaza umeme kutoka kwenye vituo na center mbalimbali na kuwapelekea wananchi kwenye vitongoji vyao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi huu nimekuwa nikiusema, unaitwa Underline Distribution Transformer ambao unaanza Julai, 2016 na utakamilika ndani ya miezi 18. Mradi huu utasambaza umeme kwenye vitongoji vyote ambapo umeme wa msongo wa kilovoti 33 umepita.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili la Mheshimiwa Mbunge ni kweli tumekuwa tukiahidi kwamba tutapeleka umeme kwenye vitongoji. Nilimwomba Mheshimiwa Kakunda aniletee vitongoji vyake vyote, ameshaleta na namshukuru sana. Kwa hiyo, napenda kumwambia Mheshimiwa Kakunda vitongoji vyake ambavyo umeme umepita vitapatiwa umeme wa uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ni lini tutatembelea, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge, kwa ridhaa yako nadhani tukishamaliza Bunge hili, niongozane na Mheshimiwa Kakunda na niwahakikishie Wabunge wa karibu na Sikonge nitawatembelea wote mara baada ya Bunge hili la bajeti.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri lakini naomba niweze kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa amekiri kwamba wananchi wako tayari kupanda miti na kuna tatizo la vitalu vya miti, je, Serikali itaweka lini bajeti na utaalam ili kusudi vitalu vya miti viweze kuoteshwa katika kila Wilaya hapa nchini ili wananchi waweze kupanda miti?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, miti mingi ambayo imekuwa inapandwa asili yake inatoka nje ya nchi siyo miti ya asili, je, ni lini sasa Serikali itaweka mkazo ili kusudi miti ambayo itaoteshwa kwenye vitalu ili wananchi waipande iwe ni miti ya asili ambayo ni rafiki wa mazingira na rafiki wa maji? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, suala la vitalu na Serikali kutenga bajeti, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya swali la msingi ni kwamba tayari tumeanza kutenga bajeti. Kwa mwaka huu kwa kuanzia tumetenga shilingi bilioni mbili na tunataka katika miaka ijayo ya fedha tuwe na wastani wa kutenga zaidi ya shilingi bilioni 20 kila mwaka ili kuweza kupanda miti inayostahili Kitaifa.
Vilevile tumesema kwamba Halmashauri zote zina jukumu pia la kutenga fedha kwa ajili ya shughuli hii na hivyo sasa katika mpango wa upandaji miti tuliouandaa wa mwaka 2016-2020 unabainisha haya na kwamba Halmashauri zote zitawajibika kuhakikisha tunakuwa na vitalu katika ngazi ya kata mpaka vijiji na kwenye taasisi kama shule ili wananchi waweze kupata miche na mbegu kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili amesema kwamba miti mingi inayopandwa ni ya kutoka nje, suala hapa siyo miti kutoka nje bali tunapanda miti yenye faida na wananchi tunawasisitiza wapande miti yenye faida. Kwa hiyo, wataalam wetu wanaohusika na misitu pamoja na hawa wa mazingira wamefanya upembuzi wa kujua kila eneo linafaa kupandwa miti ya aina gani, linafaa kupelekewa miti ya aina gani ambayo inaweza kustawi lakini vilevile yenye faida kwa wananchi kwa mfano, miti ya matunda, mbao, dawa kikubwa tumewaelekeza wataalam wetu wapeleke miti yenye faida.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Sambamba na majibu aliyotoa Mheshimiwa Naibu Waziri ninaomba awahakikishie wananchi wa Sikonge ambao wamekuwa hawaridhiki na matengenezo ya barabara ya Sikonge - Mibono hadi Kipili ambayo wakandarasi wamekuwa wakitengeneza kipande cha Sikonge hadi Mibono na kuacha kipande cha Mibono hadi Kipili bila matengenezoya aina yoyote kiasi ambacho haipitiki kila mwaka. Kwa sababu mwaka huu imepangiwa shilingi milioni 892 anawahakikishiaje wananchi wa Sikonge kwamba mwaka huu itatengenezwa kwa kiwango bora mpaka mwisho wa barabara ya Kipili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, pamoja na wananchi wa Sikonge kwamba fedha hizo zilizotengwa ni kwa ajili ya pamoja na kipande cha Mibono hadi Kipili na tutahakikisha tunasimamia ili barabara hiyo itengenezwe kwa kiwango kizuri kama ambavyo imetengenezwa eneo la Sikonge hadi Mibono.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Hapo kwenye hilo swali, napenda kuiuliza Serikali wapo wastaafu kule kwangu wengi zaidi ya 20 ambao wananifuata ofisini, ni wazee, wengine wameshafariki hawajalipwa waliokuwa watumishi wa Afrika Mashariki, waliokuwa watumishi kama Game Officers. Sasa kwa nini Serikali isiwe proactive kuwafuatilia hao wazee huko waliko ili waweze kulipwa mafao yao, badala ya kutusumbua Wabunge ambao tumeingia hivi karibuni?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Watanzania wote ni mashahidi, Wizara ya Fedha na Mipango ina zaidi ya miezi mitatu sasa ikizunguka mikoa mbalimbali kufanya tathmini na kuhakiki wastaafu wote. Kwa hiyo, hilo alilolisema Mheshimiwa Kakunda, Wizara ya Fedha ilishafika Tabora na tayari imeshafika Sikonge. Kama wapo ambao hawakufikiwa tuna utaratibu zoezi hili ni endelevu waweze kufika na kuhakikiwa na haki yao watapata bila tatizo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kunipa nafasi. Niseme wazi kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza kwamba wananchi wa Sikonge wemesikitishwa sana na majibu ya Serikali. Ninayo maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kutumia takwimu za Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) za mwaka 2012 kama zilivyo ni sahihi, lakini je, Serikali haioni kuwa kutumia takwimu hizo bila kufanya projections kwa kutumia formular rasmi iliyo kwenye taarifa ya uchambuzi ya NBS inaweza kusababisha takwimu zisizo sahihi kwa mwaka 2017 na hivyo kusababisha Bunge hili pamoja na wananchi kuamini kuwa Serikali imelidanganya Bunge pamoja na wananchi? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa kuwa takwimu rasmi zilizoko kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya ya Sikonge pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, ambazo pia ndizo alizonazo Mkuu wa Idara ya Maliasili wa Halmashauri inaonyesha kwamba kati ya kilometa za mraba 27,873 za Wilaya ya Sikonge, kilometa za mraba 26,834 ambayo ni sawa sawa na asilimia 96.3 ni hifadhi za misitu, wanyamapori, mapori ya akiba na maeneo mengine ya hifadhi ambayo yote hayo yako chini ya udhibiti na dhamana ya Kisheria ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Je, wananchi tumebaki na kilometa za mraba elfu moja na thelathini na...
…hili la pili, Serikali itateua lini timu yake ije kufanya kazi na timu yetu Sikonge, ili kusudi tupate suluhisho la kudumu kuhusu takwimu hizo?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, takwimu huwa zina chanzo, na mara nyingi unapokuwa unataka kunukuu takwimu ni lazima useme chanzo cha takwimu hizo yaani hizo takwimu ni kwa mujibu wa nani aliyezifanya. Takwimu zina mwenyewe na mwenye takwimu ni lazima awe ni mtu mwenye mamlaka na kwa Taifa hili takwimu ni mali ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, takwimu nilizozitumia kwa kuwa ni za Mtakwimu Mkuu wa Serikali sina shaka kwamba takwimu hizi ni sahihi na hizi ndizo takwimu zinazotakiwa kutumika
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kufanya projections kwamba ilitakiwa kuzitoa kutoka mwaka 2012 kuzileta leo, hiyo inaweza kuwa ni hoja, lakini ingekuwa ni hoja tu kama kweli hoja ya takwimu ingekuwa ni ya msingi kutokana na swali la msingi lililoulizwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ifahamike kabisa kwamba nchi yetu ndio nchi inayoongoza duniani kwa kuwa na eneo kubwa lililotengwa kwa ajili ya uhifadhi kwa ajili ya wanyamapori, misitu na hifadhi nyingine. Sisi tumetenga asilimia 25 ya eneo zima la nchi yetu, hiyo inatosha kutuma ujumbe kwamba ni kweli tumehifadhi maeneo makubwa. Lakini hatukufanya hivyo kwa makosa, tulifanya hivyo kwa sababu za msingi ambazo ndio zimekuwa zikitupa faida nyingi sana zinazotokana na uhifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tunapozungumzia uhifadhi kwenye eneo la Sikonge ifahamike kabisa kwamba uhifadhi huo sio kwa ajili ya Sikonge. Kila eneo lililohifadhiwa hapa nchini limehifadhiwa kwa maslahi ya Taifa. Eneo hilo litaweza kupitiwa pale ambapo kama Taifa tutaona kwamba kweli kuna haja ya kufanya mapitio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimuombe Mheshimiwa Mbunge, pamoja na kumpongeza kwamba yuko hodari wa kufuatilia masuala yanayohusu wananchi wake, na yeye atakumbuka vizuri kabisa kwamba mwanzoni mwa mwaka huu tulikuwa wote Sikonge, tumepita kwenye maeneo yake, nami napenda wananchi wa Sikonge wajue kabisa kwamba wanao jembe, Mbunge wao ni mfuatiliaji sana wa masuala yanayohusu wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati huo huo nataka nimuombe kwamba atumie fursa hiyo ya kuwakilisha wananchi kwa kuwaambia ukweli kwamba akiba ni akiba na tunatakiwa kuyahifadhi maeneo yale kama akiba. Tutaweza kuyatumia pale tu itakapotokea kwamba kuna ulazima wa kuweza kufanya vinginevyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Serikali kuteua timu, nirudie tu kwamba tayari timu ipo na iko kazini na inaendelea na kazi hiyo, kinachosubiriwa sasa hivi ni wao na ile kazi yao kukamilika na kuweza kuleta mrejesho Serikalini kwa ajili ya kuweza kupiga hatua kutekeleza masuala haya yanayohusiana na upitiaji upya wa kile ambacho tunacho hivi sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho kabisa niseme kwamba kamwe Serikali haitaweza kufikia mahali ikaamua tu haraka haraka kuweza kuyaondoa maeneo yaliyohifadhiwa kwa matumizi mengine bila kufanya tathmini ya kuangalia kwamba maeneo yasiyohifadhiwa yametumika kwa tija. Kwa hiyo, jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba maeneo ambayo hatujahifadhi yanatumika kwa tija kwanza ndipo tuanze kugusa maeneo ambayo yamehifadhiwa kwa ajili ya akiba ya Taifa hili kwa ajili ya kizazi kijacho.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba barabara ya Sikonge – Mibono – Kipili ilipandishwa hadhi tangu mwaka 2009 na hadi leo imetobolewa kwa kiwango cha kilometa 42 tu kati ya 282 ambayo ni kama kilometa tano kwa mwaka; ina maana kwamba hadi itakapokamilika barabara hiyo tunahitaji miaka 44. Je, Serikali iko tayari kuwaambia wananchi wa Sikonge kwamba itajenga barabara hiyo kwa kipindi cha miaka 44 ijayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utaratibu wa fedha za Mfuko wa Barabara zinazogawiwa mikoani kwa ajili ya matengenezo, haturuhusiwi kutumia fedha nyingi sana kwa ajili ya kutoboa barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ombi lake tunalichukua na tutatafuta namna ya kuhakikisha barabara hii kipande hiki kipya cha kukitoboa tunakitoboa kwa haraka zaidi na naomba wananchi wote wa Sikonge wachukue hiyo ndiyo kama commitment ya Serikali.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo cha FDC Sikonge kinatakiwa kutoa mafunzo katika fani za useremala, uashi, uchomeleaji, ushonaji na ufundi umeme. Kutokana na upungufu wa walimu uliopo na uchakavu wa majengo, chuo kwa sasa kinatoa mafunzo kwenye fani ya umeme peke yake. Maswali yangu mawili, je, Serikali aione kuwa chuo hiki kinahitaji jicho la kimkakati ili kukiokoa?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, katika jibu la msingi ameahidi kwamba Chuo hiki kitatembelewa, kitatembelewa lini na nani? Ahsante sana.
NAIBU WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inatambua umuhimu wa kuviimarisha vyuo hivi ili kuweza kuchukua wanafunzi wengi zaidi na kutoa mafunzo yaliyo bora zaidi kulingana na uhitaji wa soko, lakini vilevile kuhakikisha kwamba wananchi wengi zaidi wanaweza kujiajiri wenyewe. Kwa upungufu alioainisha Mheshimiwa Mbunge tutatembelea chuo hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla wake Waheshimiwa Wabunge ili tu-save muda, kimsingi mkakati ni kutembelea vyuo vyote vya FDCs ili kuona namna bora zaidi ya kuviendesha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la kwenda Sikonge nitakufahamisha Mheshimiwa, kimsingi tutaenda na kwa sababu Mheshimiwa Mbunge ni muhimu kuwepo, tutakujulisha twende wote ikiwezekana katika kipindi hiki cha bajeti katika weekend mojawapo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, ninapenda niulize Serikali; kwa kuwa uwekezaji uliofanywa kwenye kituo hicho wa shilingi bilioni 1.8 ambao ulitumika kujenga majengo mbalimbali ikiwemo nyumba sita za kisasa kabisa ambazo hata Mheshimiwa Waziri Mkuu anaweza akakaa mule, na majengo mengine. Kwa nini Serikali isiharakishe usajili upya wa kituo hicho ndani ya mwezi huu wa Septemba ili tathmini ya kina ifanyike ndani ya mwaka huu wa fedha ili kituo hiki kianze kutoa manufaa kwa vijana walio wengi zaidi?
Mheshimiwa Spika, la pili, kwa kuwa kituo hicho kilizinduliwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete mwaka 2014 na hakijaonesha sura iliyokusudiwa wakati kinazinduliwa.
Je, Serikali haioni kwamba upo umuhimu wa kuchukua hatua za makusudi za kiutawala, za kibajeti na kitaasisi ili kituo hicho kiwe na sura ile ambayo ilikusudiwa wakati kinazinduliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Spika, katika swali la kwanza la kukamilisha usajili ndani ya Septemba hii, suala la usajili ni hatua na kama Serikali ambacho tutakifanya ni kuhakikisha tu kwamba tunahimiza kazi hii ifanyike mapema zaidi ili kituo hiki usajili wake ukamilike na baadaye sasa ifanyike tathmini ambayo itawezesha vijana wengi zaidi wa Sikonge waweze kunufaika. Kwa hiyo, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba tutajitahidi kuhimiza taratibu hizi zikamilike kwa mujibu wa sheria ilivyowekwa ili zifanyike kwa wakati vijana wengi waweze kunufaika zaidi.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu bajeti na muundo wa utawala wa taasisi husika, na hasa ikizingatiwa kwamba kituo hiki kilijengwa kwa ajili ya kuwanufaisha vijana wa Sikonge, nichukue fursa hii tu kumuomba Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sababu kituo hiki kipo chini ya Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge ambayo pia Mheshimiwa Mbunge ni Diwani katika eneo husika, wachukue fursa hii kwanza kabisa kuhakikisha kwamba katika ngazi ya halmashauri wanajitahidi kuweka mipango mizuri kufanya kituo hiki kiweze kufanya kazi ili kiwanufaishe vijana.
Mheshimiwa Spika, lakini pia na eneo lingine la masuala ya muundo wa kitaasisi na bajeti pia, nashauri katika mtazamo huu kwamba ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge waone namna bora ya kuweza kulifanya hilo pia. Na sisi katika upande wa Serikali Kuu kwa sababu tunashughulika na vituo vingi vya vijana, pia tutatoa msaada wowote ambao utahitajika hasa katika kuwawezesha na kuwajengea uwezo wataalam hawa ambao watashiriki katika kutoa elimu kwa vijana katika eneo husika.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Napenda kuikumbusha Serikali kwamba kwa barabara hii kama sehemu ya trunk road ya Tabora- Mbeya michakato ya upembuzi, upembuzi yakinifu, usanifu, usanifu wa kina ilianza mwaka 1974 sasa ni miaka 43 haijakamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nipate majibu kwenye maswali mawili, la kwanza, je, Serikali iko tayari sasa kujibu swali langu la msingi lini itaijenga barabara hii kwa kiwango cha lami? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Serikali kama haitaji muda maalumu, je, haiashirii kwamba haiko tayari kuiweka kwenye mpango maalum barabara hii kuijenga kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Joseph George Kakunda kwamba Serikali mara itakapokamilisha upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa makabrasha ya zabuni zoezi la kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii litafanyika kwa sababu wakati huo tutakuwa tumejua gharama za ujenzi wa barabara hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Mheshimiwa George Kakunda tuwe wakweli na tuitendee haki sekta yetu ya ujenzi. Barabara hii ni sehemu ya barabara kuanzia Mbeya hadi Singida na tumekuwa tukifanya kipande baada ya kipande. Hivi tunavyoongea unafahamu kwamba sehemu kubwa imeshajengwa sasa tumebakiza kilometa hizi 172 tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie kwamba Serikali iko makini inafuatilia ujenzi wa barabara hii na siyo kwamba hatuko tayari kama alivyosema kwenye swali lake la pili. Kama tungekosa kuwa tayari hatungekuwa tumeanza ujenzi katika maeneo hayo ambayo tumeshayajenga.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa Serikali kujibu swali langu Na. 22 vizuri. Nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; mnara wa Airtel uliojengwa kwenye Kata ya Kipili, Kitongoji cha Madoletisa ambao haujawashwa kwa miaka miwili sasa na mnara wa Vodacom kwenye Kata ya Kilumbi ambao nao haujawashwa kwa miaka miwili hadi sasa: Je, ni lini itawashwa ili wananchi waanze kufaidika na huduma za mawasiliano?

Mheshimiwa Spika, je, Miradi ya Mawasiliano Vijijini iliyomo kwenye Mpango wa Maendeleo wa 2019/2020 ambayo orodha yake ipo kwenye randama pia kwenye kijitabu cha taarifa ya Wizara ya Julai 2019, itatekelezwa lini?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Spika, mnara uliojengwa katika Kitongoji cha Madoletisa ni kweli ni wa Kampuni ya Simu ya Airtel. Mnara huu ulijengwa kama mnara wa kupeleka mawimbi ya simu kwenda katika minara mingine ya mbali (Transmission Site). Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) uliliona tatizo la mnara huo ambapo unatumika kama transmission site bila kutoa huduma kwa wananchi waliopo Madoletisa na kuiagiza Kampuni ya Simu za Mkononi ya Airtel wauwekee vifaa vya radio ili mnara huo pia utumike kutoa huduma za mawasiliano kwa wananchi. Tumewasiliana na Airtel ili wakamilishe kazi ya kuwapelekea wananchi mawasiliano mara moja ndani ya mwezi huu wa Aprili, 2020.

Mheshimiwa Spika, Miradi ya Mawasiliano Vijijini kwenye Vijiji vya Igigwa, Migumbu, Nyahua na Tumbili kutoka Kata ya Igigwa, Vijiji vya Ipole, Makazi, Udongo na Ugunda kutoka Kata ya Ipole, Vijiji vya Kanyamsenga, Kiloleli na Mtakuja katika Kata ya Kaloleli, Vijiji vya Imalampaka na Mibono katika Kata ya Kipanga pamoja na Kijiji cha Kiyombo kutoka Kata ya kipili, havikupata watoa huduma katika zabuni ya mwezi Julai, 2019. Miradi hiyo itatangazwa tena mwezi Juni, 2020.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, naomba niulize Serikali na wananchi wa Sikonge wanasikiliza na Mkoa wa Tabora; je, baada ya kuwa Serikali imekamilisha maandalizi yote ya ujenzi wa kiwango cha lami barabara ya Ipole - Lungwa yamekamilika usanifu kila kitu. Je, sasa bado fedha na mkandarasi Serikali itaanza lini kujenga barabara hiyo ili kuunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Tabora?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Ipole - Lungwa ni kati ya barabara zinazounganisha Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Mbeya na kama alivyosema taratibu zote zimekamilika, kinachotegemewa tu ni lini itatangazwa kwa sababu sasa hivi tuko kwenye maandalizi ya manunuzi kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na kama alivyosema wananchi wake wanamsikia ni barabara muhimu inayounganisha na mkoa na mkoa, kwa hiyo ninahakika barabara hii itatengewa bajeti na taratibu za manunuzi once zikikamilika basi tutakuwa tumepata mkandarasi na itaanza kutekelezwa, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali ambayo yametolewa vizuri kwa ufasaha, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; sina tatizo na risiti za MNRT Portal, tatizo langu ni kwa nini mtozaji wa faini asipewe post maalum ili atoe risiti halali badala ya zile za kuandikwa kwa mkono?

Mheshmiwa spika, swali la pili, kwa nini Serikali isitoe mwongozo kwa halmashauri na WMAs zote ili fedha zilipwe kwenye control number maalum benki badala ya kubeba kwenye mabegi na kwenda kulipia porini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameongelea ni kwa nini tusitoe risiti za kielektroniki badala ya kutoa risiti za mkono. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi ni kwamba miongozo yote ya sasa tunayofanya ni kwamba Serikali inapokea mapato ya aina yeyote ile kutumia risiti za EFD na kwa upande wa Maliasili na Utalii tunatumia hiyo MNRT Portal ambayo ndio tunayopokelea fedha kwa kutumia control number.

Mheshimiwa Spika, suala analoliongelea Mheshimiwa Mbunge ni kwenye hizi Jumuiya za Hifadhi ya Wanyamapori ambazo zinasimamiwa na Serikali za Mitaa kupitia halmashauri na tunazieleleza sasa halmashauri kwa kuwa fedha zake za jumuiya hizi zinakaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali waangalie sasa utaratibu wa kuhakikisha kwamba malipo yote yanayotokana na faini yapitie kwenye utaratibu wa Serikali yaani EFD.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa mwongozo, mwongozo tulishautoa na utekelezaji wake unaendelea kufanyika isipokuwa usimamizi tu kama ambavyo amesema Mheshimiwa Mbunge kwamba imeonekana kuna wananchi wanabeba fedha kwenye mifuko. Tunatoa maelekezo sasa kwa halmashauri ambazo zinasimamia hizi jumuiya kuhakikisha kwamba usimamizi wa fedha za Serikali unapitia kwenye mifumo ya TEHAMA iliyoainishwa na Serikali, ambayo kwa Maliasili na Utalii tunatumia MNRT Portal ambayo inakusanya kwa kutoa control number na kwa wale wanaotumia EFD, basi Halmashauri zisimamie suala hilo ili fedha hizi sasa ziweze kufika kwenye Mifuko husika na ubadhilifu usiweze kujitokeza. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwanza naipongeza Serikali kwa majibu hayo na hasahasa kupima viwanja 56,792 katika kipindi kidogo cha miezi tisa, lakini Sikonge pale Mjini niao wananchi 2000 kwenye maeneo ya Ukanga wana viwanja 1400 na Majengo viwanja 6000 jumla viwanja 2000 kwa muda mrefu sana zaidi ya miaka 10 wanaomba hati hawajapatiwa.

Mheshimiwa Spika, sasa je, swali langu la kwanza wizara inawasaidieje wananchi wa Sikonge waweze kupata hati zao kwa haraka?

Mheshimiwa Spika, la pili je, Serikali haioni kwamba sasa hivi hapa nchini kuna uchumi mgumu kiasi ambacho wananchi wanapata shida kupata laki 150 kwenye miji ya vijiji kama Sikonge kupima kiwanja kimoja je, Serikali haioni kwamba hasa kuna wakati umefika wa kuwapa ruzuku ili waweze kupata hati zao za ardhi.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza anataka kujua tu kwamba ni lini utoaji hati utafanyika katika maeneo hayo. Tayari tulishafungua ofisi za mikoa na katika kasi ya utoaji hati sasa hivi inakwenda kwa kasi kubwa naomba nimuhakikishie tu kwamba ofisi yetu ya Tabora Mjini itakwenda kukamilisha hiyo na kwa kupitia majibu ninayotoa sasa basi wafike katika hayo maeneo mawili ndani ya Sikonge yenye viwanja 2000 ambao nasema kwamba hawajapewa hati mpaka leo, iwapo watakuwa wamekamilisha taratibu zote za umilikishaji.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anazungumzia suala la ruzuku kwamba 150,000 katika suala zima la upimaji ni gharama kubwa. Naomba niseme tu kwamba gharama hii si kubwa kama tunavyofikiri lakini pia inategemea na eneo husika maana kuna maeneo mengine mpaka sasa wanalipa 60,000 wanalipa 90,000. Wakiwa watoaji ni wachache unakuta kwamba ile gharama hata ya yule anayeenda kupima inakuwa kidogo ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuwa na watu wengi kwa wakati mmoja wanayohitaji gharama zile zinashuka kwa hiyo gharama zinashuka kutegemeana na volume ya kazi ambayo mpimaji anakwenda kufanya pale. Niwaombe wananchi kwamba suala la urasimishaji linakwenda kuisha 2023 kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kwa sababu ilikuwa programu ya miaka kumi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, waongeze kasi sasa hivi ili kazi ile iishe halafu tuendelee na upimaji wa kawaida ambao hautakuwa na zoezi la urasilimishaji ambao majengo yale yamekaa kiholela na upimaji wake unakuwa kidogo ni mgumu ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naipongeza Serikali kwa majibu mazuri sana ambayo wameyatoa hapa mbele ya Bunge, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza; miti hii inapatikana kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na maeneo ambayo hayajahifadhiwa, yakiwemo mashamba ya watu binafsi na ardhi ambayo inamilikiwa na watu binafsi. Sasa swali langu; kwa nini Serikali isitoe ruhusa maalum itakayosimamiwa na Serikali za vijiji kwenye maeneo hayo ambayo hayajahifadhiwa ili watu waruhusiwe kuvuna miti wanayoimiliki kihalali kwa ajili ya matumizi ya ujenzi wa nyumba za asili pamoja na nyumba za kisasa bila kwanza kupata vibali vile vya maliasili kwa sababu maeneo hayo hayahusiani na maliasili? Kwa sababu matumizi yale siyo ya kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; kuhusu uvunaji wa miti kwenye maeneo yaliyohifadhiwa; kwa nini Serikali isitoe elimu kwanza kupitia mikutano ya hadhara na njia nyingine za mawasiliano ili wananchi wapate ufahamu wa kutosha wa namna ya kuomba vibali ili wasiingie migogoro mara kwa mara ya kuvunja sheria za nchi? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali ipo kwa ngazi zote. Kuhusu swali lake linalosema kwa nini Serikali isitoe ruhusa kwenye maeneo yasiyohifadhiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yote ambayo yana rasilimali za misitu yanahifadhiwa na Serikali ikiwemo Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini kwenye ngazi za vijiji na maeneo ya wilaya, zinahifadhiwa na Serikali za Mitaa, zikiwemo halmashauri za wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo haya ambayo vibali vyake vinatolewa na Maliasili ni yale maeneo ambayo yanahifadhiwa na Wizara. Hata hivyo, kuna yale ambayo yanahifadhiwa na Serikali za Mitaa, vibali vyote huwa vinatolewa kwenye level ya vijiji na wilaya. Kwa hiyo wale wote ambao wanahitaji kupata vibali basi wawe wanakwenda kwenye maeneo hayo na pia watapata hivyo vibali.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu kwamba maeneo yote yanahifadhiwa, siyo kwa ajili ya kutunzwa peke yake, lakini pia na uhifadhi wa mazingira pamoja na utunzaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ameuliza kuhusu elimu; ni kweli kwamba Serikali imeendelea kutoa elimu mbalimbali kwa wananchi ili watambue umuhimu wa utunzaji wa miti. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango wa bajeti na fedha zilizoidhinishwa kipindi hiki tumeweka eneo la elimu ambalo tutapita kila maeneo ambayo yanazunguka hifadhi kuhakikisha kwamba wananchi wanapata elimu ya kutosha na namna ya kuomba hivi vibali vya ukataji miti. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ni pale ambapo Serikali imesema kwamba mwaka huu kulikuwa na kampuni nane za wazawa zimeingia mikataba na wakulima. Hadi ninaposimama hapa Bungeni mwaka huu kumekuwa na kuvunja rekodi ya kuwakopa wakulima maana yake wameuza tumbaku yao mwezi wa Tano, lakini hadi ninaposimama Bungeni hapa asilimia zaidi ya 50 ya wakulima hasa waliouza tumbaku yao kwenye kampuni hizo za wazawa hawajalipwa. Hawajalipwa kwa sababu kampuni hizo ndogo zimepata shida na changamoto katika kuuza tumbaku hiyo kwenye soko la dunia. Walikuwa wanauza kupitia Zambia, wamefungiwa huko. Walikuwa wanauza kupitia Malawi, wamefungiwa huko. Sasa je, Serikali haioni hasa kama Waziri, haioni umuhimu wa kukutana na hizo kampuni nane ili kuona namna ya kuwasaidia ili hatimaye nayo yawalipe wakulima haraka iwezekanavyo? Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, kwa mujibu wa sheria, zao la tumbaku linaendelezwa na kusimamiwa na Bodi ya Tumbaku. Tangu mwaka jana Bodi ya Tumbaku imemaliza muda wake, hadi sasa hivi inafanya kazi zake kinyume cha sheria. Hivi Serikali haioni kwamba inatakiwa iteue Bodi ya Tumbaku kesho? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, Wizara ya Kilimo imeshakutana na kampuni zote nane za Kitanzania zinazonunua tumbaku na ningeomba tu-acknowledge kazi iliyofanywa na kampuni hizi za Kitanzania katika kununua tumbaku. Tumbaku yote iliyonunuliwa mpaka msimu unakwisha ni jumla ya bilioni 86. Fedha zilizolipwa mpaka sasa ni bilioni 82, kwa hiyo, sio sahihi kwamba zaidi ya asilimia 50 kwamba wakulima hawajalipwa. Tuna-acknowledge fedha ambayo haijalipwa ya wakulima mpaka sasa imebaki shilingi bilioni nne.

Mheshimiwa Spika, la pili, kwenye eneo hili tumbaku hii iliyonunuliwa na naomba Bunge lako Tukufu lifahamu kabla ya kuleta kampuni za Kitanzania katika mfumo wa ununuzi wa tumbaku pamoja na grade zaidi ya 60 za tumbaku, kulikuwa kuna tumbaku inaitwa reject inayotupwa ambayo mkulima anaitupa shambani. Ni kampuni hizi za Kitanzania ndiyo zimeenda kuinunua mpaka tumbaku inayoitwa reject na kwa mwaka huu hakuna tumbaku iliyobaki mikononi mwa wakulima. Kunapokuwa na success story, tu-acknowledge na hili ni jambo jema. Kwa miaka mingi sekta hii imekuwa kwenye dominance ya kampuni mbili tu. Tumeingiza kampuni za Kitanzania against all efforts za international market ambazo zilituzuia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu malipo yaliyobaki na tumbaku iliyoko Malawi na Zambia, Balozi Simba aliyeko Zambia ameshafanya jitihada kwa sababu walio-block tumbaku yetu isinunuliwe Zambia ni hizi hizi kampuni kubwa zilizoko ndani ya nchi, zimetumia subsidiary companies zao kule nchi kuzuia tumbaku yetu isinunuliwe. Tatizo hili tumeli- resolve, tuko kwenye hatua za mwisho. Tumeongea na Benki ya CRDB na NMB watatoa fedha ili kampuni hizi zimalizie bilioni nne iliyobaki ambayo haijalipwa kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge lako Tukufu kusema tutaendelea ku-support kampuni za Watanzania kununua green tobacco na kui-export kwa sababu tumbaku haiwezi kugeuka kuwa chapati.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kuhusu suala la Bodi. Bodi ya Tumbaku imemaliza muda wake, ni kweli. Sisi kama Wizara tumeshapeleka mapendekezo vetting inaendelea na tumeshaomba kwa Mheshimiwa Rais ili aweze kumteua Mwenyekiti. Iko kwenye hatua za mwisho na ni interest yetu sisi kama Wizara kuhakikisha Bodi ya Tumbaku inafanya kazi yake kwa mujibu wa sheria. Sasa hivi Bodi haipo, Mkurugenzi anafanya kazi chini ya Katibu Mkuu kwa mujibu wa sheria.

Kwa hiyo, Bodi ya Tumbaku inafanya kazi chini ya DG na anaripoti moja kwa moja kwa Katibu Mkuu. Tumeshapeleka mapendekezo na tunaendelea kufuatilia Serikalini.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwa kuwa mitaala pamoja na mikopo huzalisha wahitimu na kwa sababu, Wizara hii ndio Wizara ya kisera. Kwa mujibu wa taarifa ambayo ilitolewa hapa Bungeni na Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa mwaka, kati ya ajira zilizoombwa za ualimu elfu 10, walioajiriwa kama elfu 10, lakini waombaji walikuwa zaidi ya laki moja. Maana yake ni kwamba, ukiangalia mpaka waliohitimu mwaka jana ukijumlisha pale ni zaidi ya laki moja wako mtaani hawajapata ajira. Sasa swali langu, ni kwa nini Serikali au Wizara hii wasijadili hili suala la ajira ili kuwasaidia, hasa Walimu ambao ni Walimu wa Kiswahili, waende kufundisha Kiswahili kwenye nchi za Afrika Mashariki pamoja na SADC?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajira ni suala ambalo ni mtambuka na kwa vile Mheshimiwa Mbunge anatoa pendekezo kwamba, tuweze kuangalia namna gani tunaweza tukawasaidia Walimu kwenda kufundisha kwenye nchi hizi za Afrika Mashariki na Kati na Kusini mwa Afrika, tunaomba vilevile suala hili tulichukue, twende tukaangalie hizo fursa ambazo zinatokea kwenye nchi hizo na namna gani tunaweza tukakaa kitako na kuweza kushawishi namna gani Walimu wetu ambao wamehitimu kwenye shahada mbalimbali za ualimu, hasa hizi za Kiswahili kwenye vyuo vyetu, wanaweza kwenda kutumika kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tunajua kwamba, masuala ya ajira mara nyingi sana yana-competition zake kwa sababu itakwenda kwenye usaili na watahitajika kwenda kwa ajili ya usaili huo. Kwa hiyo, hatuwezi kutoa guarantee moja kwa moja kwamba, tutafanya hivyo kwa asilimia 100, lakini nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kwamba tunalichukua, tutaenda kulifanyia kazi na kuweza kuangalia namna gani nafasi hizo zinapatikana na tunaweza kunufaika sisi kama nchi.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza, napongeza majibu mazuri ya Serikali. Labda kabla sijauliza maswali ya nyongeza, nina maelezo ya ziada kwamba eneo la Uwanja wa Ndege wa Ipole liko chini ya Ofisi ya TAWA Kituo cha Ipole cha Pori la Akiba la Ugalla. Nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa kutoka Tabora mpaka Ipole ni kilomita 100; na kutoka Koga mpaka Ipole WMA ni kilomita 90: Je, Serikali haioni kwamba kujenga uwanja huo wa ndege pale Ipole kutakuwa na faida zaidi katika kuvutia watalii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: kwa kuwa huyu mwekezaji ameshajenga uwanja mdogo pale Koga na inaonekana kabisa Serikali haina nia ya kuendeleza ujenzi wa Uwanja wa Ndege pale Ipole: Je, Serikali iko tayari kuyarudisha mashamba na ardhi ya wananchi wa Ipole waliyoitoa mwaka 1996 kwa nia njema kwa Serikali kwa ajili ya kujenga Uwanja wa Ndege, kuwarudishia ili waendelee na shughuli zao za kiuchumi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nampongeza sana Mheshimiwa Kakunda kwa kuwa mhifadhi na pia ameendelea kuhamasisha utalii, ikiwemo maeneo haya yaliyopo katika Wilaya ya Sikonge hasa katika Pori la Akiba la Ugalla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kutoka Tabora mpaka Ipole ni kilomita 100 ambazo huwa zinasaidia watalii wanaofika Tabora kuelekea katika eneo hili la WMA. Sambamba na hilo, Mheshimiwa Kakunda ameomba Serikali iweze kujenga kiwanja katika eneo la Ipole ili kurahisisha watalii waweze kupita njia ambayo ameisema ya kilomita 90.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri tu kwamba maeneo yenye uhitaji ni mengi; na kwa kuwa kiwanja cha Tabora kinatosheleza maeneo haya kwa hizo kilomita alizozisema, basi naomba wananchi au wawekezaji waliopo katika maeneo hayo, waendelee kuvumilia wakati tunaangalia namna ya kuweza kuboresha, kiwanja kidogo kilichopo katika Kituo cha Ipole ili kuwawezesha wale watalii wanaotaka kuingia kwenye hiyo WMA ama kwenda kwenye Pori la Akiba la Ugalla waweze kufika kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tu kwamba Pori la Akiba la Ugalla limeshapata mwekezaji na tayari huyo mwekezaji yupo tayari kuendelea kuboresha kiwanja hicho. Hata Serikali tutajipanga katika maeneo hayo kuhakikisha kwamba tunaboresha viwanja hivyo ili kurahisisha watalii waweze kufika katika maeneo hayo. Ahsante (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa kuna malalamiko mengi sana ya wananchi kwa ajili ya kuruhusiwa uwindaji wa kienyeji, kwa nini Serikali sasa isiharakishe huo mchakato wa mapitio ya Kanuni usiku na mchana ili wiki ijayo waweze kutoa hicho kibali?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato umeshakamilika na hivi sasa uko kwenye level ya Waziri, wakati wowote tutaweza kutoa mapendekezo au maelekezo ya utekelezaji wake.(Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spikaa, nakushukuru sana. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge imeshafanya tathmini kuhusu mahitaji ya maeneo ya kujenga vituo vya afya ambako kuna watu wengi na ni mbali. Kituo cha Afya katika eneo la Kata za Igigwa, Kiloleli, Ipole na Usunga. Je, ni lini Serikali itatusaidia kujenga vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka utaratibu wa kuainisha maeneo yote ambayo ni ya kimkakati kwa ajili ya kujenga Vituo vya Afya kwenye Kata na Tarafa za kimkakati na nakumbuka Mheshimiwa Mbunge alikwisha wasilisha kata hizo kwa ajili ya kujenga hivyo vituo vya afya na sisi tunafanya tathmini kujiridhisha tu na vigezo vile, lakini nimhakikishie kwamba tunafahamu Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge ni moja ya halmashauri kubwa na ina umbali mkubwa kati ya kata na kata, hivyo tutaweka kipaumbele katika ujenzi wa vituo hivyo vya afya.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na pia napongeza majibu mazuri ya Serikali hasa hiyo tathmini ambayo inaenda kufanyika ni tathmini nzuri ya school mapping.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili. Swali la kwanza, hivi karibuni kuanzia miaka ya 2017 kumekuwa na ujenzi wa madarasa, mabweni na kadhali na hiyo ni miundombinu ya shule. Je, tuna uhakika gani kama hizi Shilingi Bilioni 230 nazo zitaendeleza tu utaratibu huo wa kujenga madarasa badala ya shule mpya?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwenye taarifa ya jana ya sensa, katika Wilaya ya Sikonge, wananchi wameongezeka mara mbili, maana yake ni kwamba hata idadi ya wanafunzi imeongezeka mara mbili.

Je, kwa nini Serikali isiweke kipaumbele ya kujenga shule mpya Nne katika Wilaya ya Sikonge kwenye hayo maeneo ambayo nimeyataja kwa mwaka huu wa fedha? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge, kwamba katika tathmini tunayoifanya ya ujenzi wa shule mpya za msingi na katika fedha ambayo imetengwa sehemu ya hiyo fedha itakwenda kujenga shule mpya sehemu nyingine tutakwenda kukarabati maboma ya madarasa ambayo yamekwisha muda wake, na maeneo mengine tutabomoa kabisa na kuanza upya ujenzi katika mabwawa ambayo yamekwisha kabisa. Kwa hiyo, huo ndiyo mpango wa Serikali ambao upo, kwa hiyo nimuondoe hofu kwenye hilo.

Mheshimiwa Spika, suala lake kuhusu shule nne mpya za msingi, nikuhakikishie tu fedha ipo kwa sababu mradi peke yake wa BOOST ambao tunautekeleza kwa miaka mitano, thamani yake ni trilioni 1.15. Kwa hiyo ni fedha ipo ya kutosha ambayo tutahakikisha changamoto ya elimu msingi tunazimaliza nchini. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mji wa Sikonge unategemea sana Bwawa la Maji la Utyatya ambalo lilijengwa mwaka 1959, kuna uchafuzi mwingi kwa kipindi kirefu, uchafu mwingi umeingia kwenye hilo bwawa. Mwaka 2017/2018 Serikali ilipanga shilingi milioni 400 kwa ajili ya kulisafisha hilo bwawa, lakini haikuleta fedha kwa sababu kuna maeneo ambayo yalitakiwa Halmashauri iweze kuyalinda vizuri na mpaka sasa hivi yameshalindwa vizuri.

Je, hizo fedha zitakuja lini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, chanzo hicho tutaendelea kuja kukifanyia kazi na Bonde husika tayari limeshapewa maagizo. Nami kwa kupitia Bunge lako tukufu naomba niendelee kusisitiza Wakurugenzi wote wa Mabonde waweze kuwajibika kwa sababu vyanzo hivi ni mkakati wetu kama Wizara kuona kwamba, tunavilinda ili viweze kutuletea uendelevu wa miradi ambayo tunaendelea kuijenga. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Mkoa wa Tabora hadi leo haujaunganishwa na Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe; na kipande muhimu kabisa ambacho kinaunganisha mikoa mitano ni kipande cha kutoka Ipole mpaka Rungwa ambacho usanifu wa kina ulikamilika na tayari shilingi bilioni tano zikatengwa mwaka huu.

Ni lini hiyo barabara itajengwa ili Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Mbeya na Songwe ziunganishwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kipaumbele ni kuunganisha mikoa na mikoa na barabara aliyoitaja siyo tu kwamba ni mkoa, lakini pia ni kati ya zile barabara kuu kutoka Tabora - Ipole hadi Rungwa ambayo inaunganisha na barabara inayotoka Manyoni - Singida kwenda Makongorosi.

Mheshimiwa Spika, kipande cha Manyoni - Itigi kuja Rungwa tunategemea muda wowote kutangazwa; na kipande cha Ipole kuja Rungwa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami ili barabara hiyo ambayo inaunganisha siyo tu na Tabora, ila na mikoa mingi ya Kaskazini iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ningependa niongeze hapo swali la nyongeza, kwa kuwa Serikali imekiri hapa kwamba shule nyingi zimezidiwa na wanafunzi kwa nini Serikali sasa isitangaze kwamba hapa Tanzania tuna upungufu wa shule badala ya kuendelea kutangaza kwamba tuna upungufu wa madarasa peke yake?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Kakunda Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la Mheshimiwa Mbunge tu ni kwamba anataka kufahamu tutangaze kwamba tuna uhaba wa shule na siyo madarasa. Nimhakikishie tu kwamba Serikali inatambua changamoto zote, katika baadhi ya maeneo tuna changamoto ya madarasa na kuna baadhi ya maeneo tuna changamoto ya shule, ndiyo maana katika maeneo ambayo yana changamoto ya shule Serikali tunapeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya, kwa hiyo hatuwezi kutangaza kama janga kwa sababu Serikali ipo kazini na inafanya kazi kutatua hizi changamoto ambazo Mheshimiwa Mbunge ameainisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Katika Jimbo langu la Sikonge, mwaka jana baada ya tathmini kufanyika kila kijiji kwa kushirikiana na Viongozi wa Vijiji, kuna orodha ambayo ilikubalika kwa pande zote mbili, lakini ilipofika Makao Makuu ya Wilaya wakapunguza idadi kwa nusu. Hao waliopunguzwa wana malalamiko makubwa sana dhidi ya uamuzi wa kuwaondoa kwenye orodha ya wafaidika wa TASAF. Je, Serikali kwa nini ilichukua hatua hiyo na itarekebisha lini hatua hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu uliokuwepo ni kwamba yale majina ambayo yote yanaondolewa imewekwa namna ya kukata rufaa kwa yeyote ambaye anaona anakidhi vigezo vya kuwepo kwenye Mpango huu wa TASAF. Hivyo, nashauri kwamba watu wa Sikonge ambao wanaona kwamba wanastahili kuwepo kwenye mpango huu waweze kukata rufaa na rufaa zile zinapelekwa TASAF Makao Makuu. Inatumwa timu ya wataalam kuweza kwenda kuhakikisha na kuona kama watu hao wanastahili na kuweza kurudishwa kwenye mpango. Vile vile kama kwa Mheshimiwa Migila nitakaa na Mheshimiwa Kakunda ili kuona jinsi ya wataalam wetu kuweza kwenda na kuiangalia hiyo tathmini kwa ujumla.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Katika Jimbo la Sikonge wananchi wangu wanaendelea kuamini kwamba katika Mlima wa Kipanga, Milima ya Kisanga na Mapori ya Ipembampazi kuna madini; na hili suala limeulizwa tangu enzi za Mheshimiwa Said Nkumba akiwa madarakani.

Je, Serikali itakuja lini sasa kuja kufanya utafiti ili kuitikia wito wa wananchi kwamba kule kuna madini?
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba yapo maeneo mbalimbali Mkoa wa Tabora ambayo yanaaminika kuwa na madini na bahati mbaya hayajafanyiwa utafiti wa kina. Taasisi yetu ya utafiti GST iko katika Mikoa ya Kusini. Nataka nimhakikishie, baada ya kumaliza mzunguko wa Kanda ya Kusini tutawapeleka na Mkoa wa Tabora, ikiwemo eneo la Sikonge ili waweze kufanya utafiti wa awali.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, natambua kwamba watoto ambao wanazidi miaka mitano na wengi wao ni wale ambao wana Selimundu wamekuwa wakitozwa fedha katika hospitali ikiwemo hospital za Serikali.

Swali la kwanza, je, kwa kuwa hadi sasa Serikali inagharamia dawa za magonjwa kama UKIMWI, kifua kikuu na ukoma; kwa nini Serikali isiingize kwenye bajeti matibabu ya Selimundu kwa wagonjwa wa Selimundu ambao ni wachache kwenye bajeti ijayo kuanzia mwezi Julai?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa kuwa dawa zinazotibu Selimundu ikiwemo hii dawa inayoitwa hydroxyurea zimekuwa hazipatikani kwenye Wilaya nyingi ikiwemo Sikonge hali ambayo wagonjwa wanalazima kusafiri kwenda sehemu za mbali kama Mwanza au Dar es Salaam; kwa nini dawa hizi zisiletwe kwenye Wilaya ili zipatikane katika Wilaya kuondoa usumbufu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, labda nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia hili suala kwa ukaribu, lakini swali lake la kwanza kwamba ni kwa nini tusitenge bajeti?

Mheshimiwa Spika, Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan amefika mbali kwenye hili kwamba sasa kuna tiba ambayo inafanya gene editing kwa kutumia CRISPR-CAS9 technology ambayo ameshatafuta shilingi bilioni 11.5 kwa ajili ya kuanza, siyo tu kutibu kwa kupeleka dawa, lakini sasa kwenda kwenye genetic makeup ya mtu na kufanya diting ili kuweza kumtibu huyu mtu moja kwa moja na tiba hiyo siyo muda mrefu itaanza.

Mheshimiwa Spika, pia tutaona kwenye baadhi hospitali zetu za mikoa sasa zimeanza kutenga asilimia 10 ya bajeti yao mapato yao ya bima kuwasaidia watu hawa na ndiyo maana wakati wote tumekuwa tukiwasisitiza ninyi Wabunge tukikubaliana kwamba tutafika kwenye Bima ya Afya kwa Wote ni moja ya suluhisho hili la kutatua hili tatizo.

Hivyo Mheshimiwa Mbunge nakubaliana na wewe ni wazo zuri kutenga kwenye Bajeti.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, nimepokea wito wa Serikali kwamba tuendelee kushirikiana na wananchi kujenga shule; na kwa kuwa mwaka jana tulileta maombi ya kujengewa/kumaliziwa shule 58 za shikizi tukapata shule kumi tu kati ya 58 bado shule 48 zimeongezeka sasa hivi ziko 55.

Je, Serikali itatupatia lini fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa shule hizo shikizi 55 ambazo zipo sasa hivi? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, usajili wa shule za msingi na usajili wa shule za sekondari hufanywa kwa mikondo, mkondo mmoja wa shule za msingi una watoto 45 na mkondo mmoja wa shule za sekondari nadhani una watoto 40. Sasa maana yake ni kwamba shule yenye mikondo minne inatakiwa iwe na wanafunzi kwenye darasa moja wanafunzi 180 katika shule ambazo zimeshazidi idadi ya wanafunzi wanaohitajika kwenye mikondo. Kwa nini Serikali isiwe na mkakati maalum wa kitaifa wa kujenga shule mpya karibu na maeneo ambayo shule zimezidi idadi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mbunge kwamba moja ya mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kwamba tunamalizia shule shikizi zote na kwa awamu ya kwanza katika mwaka wa fedha huu hapa ambao tupo, Mheshimiwa Rais alitoa fedha na tukajenga madarasa 3000 nchi nzima kwenye maeneo ya shule shikizi.

Kwa hiyo, hizo shule kumi ambazo tulileta katika maeneo yako, na sasa hivi tuna mipango mingine ambayo tuna fedha, na baadhi ya fedha tutazielekeza katika maeneo ambayo bado yanaupungufu na yana mahitaji hususani katika shule shikizi, kwa hiyo, katika kipaumbele tutakachotoa ni pamoja na hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba tunatapisha shule zote ambazo zina wanafunzi wengi na ikiwemo kusajili katika maeneo ambayo sasa idadi ya wanafunzi ni kubwa hususani katika hizi shule shikizi ambazo zimezidi.

Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge haya yote yapo katika mpango wa Serikali na tunaendelea kuyatekeleza na mfano mzuri katika mwaka huu wa fedha na katika bajeti ambayo tumeipitisha hapa ya mwaka 2022/ 2023.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Hili linahusu Majimbo yote ya Vijijini hasa hasa kule ambako kumejengwa shule shikizi, nyumba nyingi za Walimu zilizopo zimejengwa kwenye maeneo ambayo angalau Mwalimu anaweza akapata nyumba za kupanga, sasa hizi shule ambazo ziko kwenye maeneo ambayo Mwalimu hapati hata nyumba za kupanga.

Je, kwa nini hizo shilingi bilioni 43 zisielekezwe kwenye maeneo kama hayo badala ya kuangalia maeneo mengine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa George Kakunda Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nilipokuwa najibu swali nimeainisha kwamba maeneo ambayo tutayazingatia zaidi ni maeneo yenye uhaba, maeneo ya pembezoni kwa hiyo ni moja ya jambo ambalo sisi tumelizingatia. Ahsante sana.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza niseme tu ukweli kwamba, Mheshimiwa Naibu Waziri ni miongoni mwa viongozi wakweli sana. Sasa naomba Mheshimiwa Naibu Waziri au Serikali ituambie, kwenye ule Mradi wa Miji 28 bomba kutoka Tabora kwenda Sikonge litaanza kulazwa lini? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikushukuru kwa pongezi. Kwenye hii mijii 28 hivi karibuni tunamtarajia Mheshimiwa Rais aweze kushiriki katika kusaini ambapo sasa kazi zitaanza na bomba hilo litalazwa mara baada ya mradi huu kuanza kufanyiwa kazi.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa kuwa uamuzi wa mwisho wa Serikali kugawa halmashauri, wilaya na mikoa ulifanyika mwaka 2012, takribani miaka kumi iliyopita, na kwa kuwa maeneo mengi sasa hivi yana sifa kabisa za kugawiwa, mfano Mkoa wa Tabora, Morogoro, Tanga na mikoa mingine mikubwa na baadhi ya wilaya ambazo ni kubwa kama Sikonge na Mbeya.

Je, maamuzi mengine ya Serikali tuyategemee lini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA
MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephat Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa Kwamba Serikali ilifanya maamuzi ya mwisho, mwaka 2012, na muda ambao umepita mpaka sasa hivi ni miaka kumi na bado Serikali inapitia na kutathmini kuona haja ya kuongeza endapo maeneo ya utawala, ama tuendelee na sasa ili tuendelee kuyaboresha na kuwa bora. Kwa hiyo, naamini kabisa Serikali uamuzi wake mpaka sasa hivi upo sahihi na bado tunazingatia; na siyo kwamba mwaka 2012 ndiyo ilikuwa mara ya mwisho. Bado huo mchakato utaendelea baada ya kuona mahitaji ya wakati wa sasa. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana; Wilaya ya Skonge tangu ianzishwe mwaka 1996 OCD amejibanza kwenye vijumba ambavyo vilianzishwa na Mtemi Haruna Msagila Lugusha, 1957, havitoshi na havifai;

Je, Wilaya ya Skonge itajengewa lini kituo cha polisi cha Wilaya chenye hadhi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Kakunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuungane naye kwamba baadhi ya majengo yanayotumika na polisi si yale yaliyojengwa na Serikali bali ni yale yaliyotolewa na wadau waliokuwa kwenye maeneo hayo miaka kadhaa iliyopita. Sasa kupitia Bunge lako Tukufu nimwombe IGP kupitia RPC wake wa Mkoa wa Tabora waweze kufanya tathmini ya eneo hilo la kibanda anachosema kinakaliwa na OCD wa Sikonge kuangalia kiwango gani cha ukarabati tunahitajika kufanyika ili tukitengee fedha kikarabatiwe kikidhi mahitaji ya OCD, nashukuru.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa Bwawa la Olua ambalo lilizinduliwa na Mwalimu Nyerere tarehe 15 Julai, 1977, yeye mwenyewe aliahidi kwamba atatoa eneo kwa ajili ya scheme ya umwagiliaji kwa kutumia maji ya bwawa hilo.

Je, ahadi ya Rais tangu lini ilifutwa?

Swali la Pili; kwa kuwa Mawaziri sita wa Maliasili wameshalitembelea eneo hilo tangu mwaka 2010 na Waziri wa mwisho alikuwa Mheshimiwa Dkt. Hamis Kigwangalla mwaka 2019: -

Je, ni lini ahadi ile ya Mheshimiwa Rais na ahadi ya Waziri wa Maliasili itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nirejee tu kwenye jibu langu la msingi kwamba maeneo haya yanapokuwa yameombwa mara nyingi wataalam wanaenda kuhakiki na wanaangalia kama kuna maeneo ambayo ndani yake kuna wanyama wakali na waharibifu hususani tembo, pia tunaangalia vitu mbalimbali ikiwemo masuala ya ikolojia wataalam walipoenda kuangalia walikuta umuhimu wa maeneo haya kuendelea kuhifadhiwa, na hii ahadi iliyotolewa ilikuwa ya mwaka 1977, tunatambua kabisa hifadhi hizi zinasimamiwa na Halmashauri lakini pale ambapo kunakuwa na umuhimu wa kuwaachia wananchi basi Serikali inafanya tathmini na inarejea na kuwarudishia wananchi waendelee kuyatumia kwa ajili ya shughuli nyingine.

Mheshimiwa Spika, naendelea kumuomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi bado ipo, tathmini itaendelea kufanyika na pale ambapo tutaona kuna umuhimu wa kuyarejesha haya maeneo basi tutafanya hivyo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Ni lini wananchi wangu wa Kata za Pangale, Mpombwe, Tutuo, Sikonge, Mkolye hadi Ipole watapata fidia ambayo wamepisha njia ya kupita umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inajenga laini ya kilovoti 33 ya kupeleka Gridi ya Taifa Katavi ambapo inatokea Kituo chetu cha Tabora inapita Ipole ambako ndiko katika jimbo lake, inakwenda Inyonga na baadaye inafika Mpanda Mjini.

Mheshimiwa Spika, laini yote hiyo ina jumla ya kilometa
380 na pesa zimeshapatikana kwa ajili ya kulipa fidia, na mkandarasi anaingia site karibia kwenye mwezi Julai au Agosti. Kabla ya muda huo fidia itakuwa tayari imelipwa ili Gridi ya Taifa iweze kufika Katavi na wananchi wake wataweza kulipwa fidia ambayo wanastahili kupewa.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahadi ya Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu ni kuiunganisha Kata ya Nyahua na Makao Makuu ya Wilaya ya Sikonge na zilitengwa bilioni 1.86 mwaka juzi na mwaka jana, lakini haijatoka hata senti moja. Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza hiyo ahadi kwa kutoa hizo fedha ambazo zilitengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeshawajibu Waheshimiwa Wabunge wengine hapa kwamba, kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutakaa na wenzetu wa TARURA kuona ni namna gani wamejipanga katika utekelezaji wa ahadi hii.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza la kwanza baada ya ziara ya mawaziri nane kwenye maeneo yetu ya Wilaya Sikonge. Serikali ilituma timu ya watalamu ambao ilifanya kazi na viongozi wa vitongoji, vijiji na kata na mimi kazi hiyo waliyoifanya narizika. Kwa sababu waliweka mipaka na rangi kwenye hiyo mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo ambayo nitayataja Luseseko, Isenga na Manzagata, Misulu, Simbaudenga, Ngakaro, Kawemimbi na Manyanya ya 2,567 zina wakazi 25,000. Sasa swali la kwanza je, ni lini hasa kwenye maeneo haya yenye wakazi wengi watakuja kuweka bikoni ili kuwaondolea wasiwasi wananchi wangu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kwa kuwa uamuzi wa Serikali wa mwaka 2019 uliondoa zile mita 500 za bafa zone ambazo zilikuwa chini ya hifadhi kipindi kile sasa zikawa chini ya halmashauri ili waweze wananchi kuzitumia je, hizo mita 500 kuzunguka maeneo yote ya hifadhi wananchi watakabidhiwa lini kwenye halmashauri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza suala la lini hasa bikoni zile zinaenda kuwekwa, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika eneo lako watalamu wanakwenda kuendelea na shughuli hizi. Kwa sababu mpaka sasa watu wako uwandani wanaendelea na kazi. Kitu cha msingi kikubwa kuweka msukumo mkubwa ambao watawezesha sasa alama zote katika maeneo husika ziweze kufikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote katika maeneo yenu yanayopitiwa na hii miradi tuwaombe wananchi wawe watulivu sana katika zoezi hili kwa sababu wakati mwingine linapotoshwa katika ile tafsiri halisi wakati utekelezaji umesimama imara kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; hii bafa zone ambayo tumeiyondoa katika maeneo yetu, wakati zoezi la upimaji wa vijiji unao endelea ndiyo wakati ambao utabainisha hizi mita 500 za eneo ambalo zinatakiwa zirudishwe kwenye halmashauri, naomba tu tuwe watulivu wakati zoezi hili likiendelea, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Mimi nimemsilikiza sana Mheshimiwa Waziri na nimemuelewa lakini nataka niiambie Serikali kwamba akina Simbachawene kule Sikonge wako wengi tu na akina Lusinde na wakina Mpangala. Kwa hiyo, suala siyo kabila au asili ya mtu, suala ni anuani. Kwa nini anuani zile zisitumike kuweka wazi kwamba huyu anuani yake ni P.O.Box 8 – Sikonge, ukawa na watu labda 20 ambao umewaajiri kutoka Sikonge ukaonesha pale, kwa nini isiwe rahisi namna hiyo badala ya anavyofikiria ukabila na mambo mengine? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA N AUTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimesema kwenye jibu langu la msingi, nataka aniseme tu Mheshimiwa Kakunda alichokisema ni kwamba tuende kwenye anuani. Tukienda kwenye anuani pia kuna confusion bado, bado utaiona tu confusion kwa sababu utaichukua anuani, unataka kumchukua mtu aliyetoka kwenye Jimbo anakotoka Mheshimiwa Kakunda, lakini utatumia chuo alichosoma, utatumia mahali alikokulia, utatumia anuani alikoombea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, so kuna mambo mengi ya kuyaangalia ndiyo maana tunasema huo mfumo tunaouangalia na ushahidi tunaoungojea wa kitaalamu na utafiti unaofanyika utatusaidia zaidi kuliko hapa sasa hivi nikisema tutafata utaratibu huu. Nadhani mtuachie Serikali tulifanyie kazi tunaweza tukaja na kitu kizuri zaidi. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, napenda kuuliza: Ni lini Serikali itamaliza kabisa malalamiko ya wastaafu wa zamani wakiwemo wale wa Jumuiya ya Afrika Mashariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, ahsante. Masuala yote ya wastaafu tumeendelea sana kuboresha katika kuwasikiliza na pia kutatua changamoto zao. Hili suala la wastaafu wa Afrika Mashariki lilikuwa ni suala la kimahakama na Mheshimiwa kama unavyofahamu maamuzi ya Mahakama ndiyo huzingatiwa. Kwa hiyo, tutaangalia, wapo wengine ambao walikuwa kwenye hatua ya kufanya execution of decree ambayo ilitolewa na Mahakama na kulikuwa kuna hatua mbalimbali za kwenda kudai mafao hayo kwa waajiri. Kwa hiyo, liko katika utaratibu wa usukumwaji na ufuatiliaji kwa mfumo wa kimahakama, lakini kwa yale ambayo yamekuja upande wetu, tutaendelea kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, kama kuna issue substantial na specific kwa wastaafu kwenye eneo na jimbo lako, nitapenda nizipate ili tuzifanyie kazi. Kwa wote waliowahi kuleta, tumezifanyia kazi. Kwa hiyo, nawaomba sana, badala ya kusubiri, basi tutumie fursa hii kuweza kufanya hiyo kazi na kwenye semina ambayo tutaitoa tena kwa mara ya pili, itatusaidia sana kuweza kupata picha ya pamoja na kutatua changamoto hizi, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Ningependa kuiuliza Serikali, wakati tunasubiri utekelezaji wa mikataba iliyosainiwa mwezi Juni, je, kuna mpango gani wa kuongeza nguvu minara ambayo ipo, ambayo ina nguvu ndogo sana inayotoa mawasiliano kwenye maeneo madogo sana?
WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye bajeti iliyopitishwa hapa Bungeni ya mwaka 2023/2024, bajeti imepitishwa ya kuongeza nguvu ya minara 388 kwa ajili ya kuiongezea nguvu kama ambayo Mheshimiwa Mbunge ametoa ushauri. Naamini maeneo anayoyataja yanaweza kuwa sehemu ya hii 388 na kama hayamo, bado kuna fedha nyingine kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kuongeza uwezo wa minara ambayo tunayo ili tuachane na huduma ya 2G tuende kwenye 3G, 4G na sasa 5G.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, kule Sikonge tunayo minara kama mitano hivi ambayo ina nguvu ndogo sana yaani coverage yake ni eneo dogo sana. Je, ni lini Serikali itaelekeza haya makampuni waboreshe coverage ya minara yao hasa kwenye Kijiji cha Ibumba?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa kuna timu ambayo iliundwa na Mheshimiwa Waziri na inazunguka kufanya tathmini ili kujiridhisha na changamoto zilizopo.

Mheshimiwa Spika, kuna minara ambayo ilijengwa miaka ya nyuma ambapo mahitaji yake ilikuwa watu labda 2,000 au 3,000. Sasa unakuta kwamba katika eneo fulani kuna ongezeko la wakazi 5,000 mpaka 6,000 kiasi kwamba inazidiwa. Kuna miradi mingine ambayo changamoto yake ni masafa, lakini kuna miradi mingine changamoto yake ni teknolojia iliyotumika. Kwa hiyo timu hii inapopita na kujiridhisha chanzo cha tatizo ni nini, ili Serikali ikachukue hatua stahiki kulingana na tatizo la eneo husika. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Kakunda eneo lake tayari alishanijulisha na tayari tumeshaliweka katika utekelezaji wa utafiti huo. Watakaporudi wataalam wetu tutajua kwamba tunaenda kuchukua hatua gani ili tutatue tatizo kulingana na hali halisi iliyopo katika eneo husika, nakushukuru sana.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, kwa miaka 14 tangu NIDA ianze kazi, pale Sikonge waliopatiwa vitambulisho ni watu 61,000 tu kati 91,000 ambao walipigwa picha, maana yake ni kwamba kuna watu 30,000 hawajapatiwa vitambulisho, sasa nina maswali mawili ya nyogeza.

Je, Serikali ina mkakati gani katika kipindi cha miezi sita itawapatia vitambulisho watu wengi hivyo 30,000, wakati wastani kwa mwaka imekuwa ni 4,300? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa bado tuna watu karibu 60,000 hawajapigwa hata picha na siku hizi kuna masharti, ukienda leseni unaambiwa sharti la NIDA na huduma nyingine.

Je, kwanini Serikali haioni umuhimu wa kuahirisha hayo masharti mengine ili wananchi wasiendelee kudaiwa kitambulisho cha NIDA wakati haiwezekani kupata? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, kuhusu swali la kwanza, uhakika ndani ya miezi sita kwamba tutakamilisha upatikanaji wa vitambulisho kwa wananchi ambao hawajapata, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako tukufu kwamba katika utekelezaji wa shughuli za Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa nadhani Wabunge wote mnafahamu kwamba kwa miaka karibu mitatu hadi minne, mkataba ulikuwa umekuwa frustrated kwa sababu mkandarasi alikuwa anadai muda mrefu na madai yake yalikuwa hayajalipwa. Kwa dhamira njema ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan tatizo lile amelikwamua, ametoa fedha tukalipa madeni tuliyokuwa tunadaiwa na uzalishaji wa vitambulisho umeanza.

Mheshimiwa Spika, tulichofanya kama Wizara ni kumsisitiza mkandarasi, kwa sababu kuna wananchi wengi walikuwa wanasubiri vitambulisho hivi, awe na mpango wa kasi wa kuzalisha na namshukuru Waziri wa Mambo ya Ndani aliniruhusu nikaenda mpaka kwenye kiwanda, nimejiridhisha kuwa uzalishaji unaenda kwa kasi kubwa. Ndiyo maana tuna uhakika kwamba ifikapo Machi, wananchi wote ambao walikuwa hawajapata vitambulisho watapata vitambulisho hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nimwondoe mashaka Mheshimiwa Mbunge. Tumeanza kuimarisha utendaji wa NIDA. Baada ya uzalishaji wa vitambulisho kuanza, NIDA imepanua uwezo wake kwa kuazima staff kutoka kwenye vyombo vyetu vingine vya usalama ili kuongeza kasi ya kuwafikiwa wananchi, waweze kupata zile namba za utambulisho.

Kwa hiyo, badala ya kusitisha zoezi zile, ngoja liendelee lakini tutaongeza idadi ya watu ili wananchi wako wa Sikonge ambao hawajapigwa picha na kupewa namba za utambulisho waweze kufanyiwa hivyo, nashukuru. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ningependa kuuliza kuna vituo vya afya vingi nchini ambavyo havijamaliziwa OPD. Ni lini OPD zitamaliziwa katika vitu vya afya ambavyo havina OPD?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa awamu katika halmashauri mbalimbali hapa nchini kwa ajili ya umaliziaji wa majengo haya. Tunaendelea kutafuta fedha kuona ni namna gani tunapeleka kwa ajili ya umaliziaji wa majengo ambayo bado hayajakamilika. Na kwa yale yaliyokamilika Serikali inaendelea pia kupeleka vifaa tiba ili huduma kwa wananchi iweze kuanza kutolewa kwa wakati.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Nami naomba niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kijiji cha Majengo, ramani ya umeme imepeleka umeme kwenye kitongoji cha Nshepa badala ya makao makuu ya Kijiji. Je Serikali iko tayari kutoa maelekezo katika vile vitongoji 15, makao makuu ya Kijiji cha Majengo yapelekewe umeme mwaka huu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitongoji 15 ambavyo tumepata pesa jumla ya shilingi bilioni 357 kwa ajili ya kuongeza vitongoji 15 kwa kila Jimbo, tulisema juzi katika bajeti na nirudie tena, litakuwa ni chaguo la Mheshimiwa Mbunge mwenyewe kuchagua ni wapi hivyo vitongoji 15 apelekewe. Kwa sababu kama anavosema Mheshimiwa Aweso kwamba anayelala na mgonjwa ndiye anajua mihemo yake, tunaamini Waheshimiwa Wabunge mnatambua zaidi mahitaji yako wapi kutuzidi sisi. Kwa hiyo, tuyashirikishana pamoja na ninyi kujua na kutambua ni maeneo gani ya vitongoji viwe vya kipaumbele wakati tukiwa tunaelekea kupata pesa nyingi ili kumaliza vile vitongoji 36,101 ambavyo bado havijapatiwa umeme. (Makofi)
MHE. JOSEPH. G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, maeneo kama Mwamayunga, Isongwa, Ipembe, lini nayo yatapata minara ya simu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANONA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kata ambazo amezitaja tayari tumeziweka kwenye tathmini katika vijiji 2224 na tayari Mheshimiwa Rais ameshapata fedha kwa ajili ya minara 600 na baada ya 600, kuna minara mingine 1,000 inakuja, kwa hiyo tukitoka hapa leo tukae Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kuyapanga vizuri kwa ajili ya wananchi wa Jimbo lake ili waweze kupata huduma ya mawasiliano, ahsante sana.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana majibu ya Serikali yamekuwa mazuri. Lakini kwa hali ya Jimbo la Sikonge ilivyo, kilometa za mraba 27,873, kuna wananchi wanatembea kilomita 70 mpaka kilometa 100 kufikia kituo cha afya cha karibu; je, Serikali haioni kwamba Wilaya au Jimbo kama la kwangu wanatakiwa waweke kipaumbele maalum ili watu wasiwe wanatembea kilomita 100 kufata kiyuo cha afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili hizo fedha ambazo nimeuliza mimi bilioni 1.5 ni ela kidogo sana kwa Serikali; je, lini watatupatia hizo ela ili tuanze na hivyo vituo vitatu tulivyopendekeza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kakunda Mbunge wa Sikonge, la kwanza la Serikali kuona umuhimu. Serikali inaona umuhimu wa kujenga vituo vya afya kote nchini na ndio maana Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ilijenga vituo vya afya 234 kwa kutumia zaidi ya bilioni 117 kwa ajili ya kupeleka huduma karibu na wananchi. Tutakaa kuona ni mipango ipi iliyowekwa katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya kujenga vituo vya afya katika Wilaya ya Sikonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili, tutaangalia kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuona tunapataje fedha hii kwa ajili ya kusogeza huduma karibu kule Jimboni Sikonge.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza niishukuru sana Serikali kwa usikivu na kusikia ushauri wetu sisi Wabunge, kama ilivyo kwenye Ibara ya 63(2), nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu; je, Serikali itakuwa tayari wakati wanapokamilisha hiyo rasimu ya sheria kunikaribisha na mimi nitoe maoni yangu moja kwa moja?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kama ilivyo ada ambapo utungaji wa sheria unahusisha wadau mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wabunge na Kamati yako ya Kudumu ya Bunge, Mheshimiwa Mbunge kwa kweli ataalikwa na atashiriki katika hata hatua za mwanzo hadi sheria itakapokamilika, nashukuru. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza; kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri kabisa ambayo yamekwenda shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa taarifa ya sensa ya mwaka 2012 nchi yetu ina jumla ya nyumba 11,873,1950; kati ya hizo, nyumba bora ni 3,444,519 sawasawa na asilimia 37.1 maana yake tuna nyumba 8,429,431 ambazo ni sawa na asilimia 62.9 nyumba hizi sio bora, lakini kati ya hizo nyumba 2,359,906 sawasawa na asilimia 25.4 ni nyumba zimeezekwa kwa nyasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu; nyumba ya kawaida ya vyumba viwili inahitaji shilingi 400,000 kwa maana ya kununua bundle mbili za mabati. Je, kwa nini Serikali isiweke pale shilingi 200,000 kwa mtu ili na yeye achangie shilingi 200,000 ili hatimaye Serikali itumie kama shilingi bilioni 432 kuondoa kabisa nyumba za nyasi katika nchi hii? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; ni kwa nini Serikali isiweke viwango vya nyumba bora, ili kila mwananchi awe anazingatia ujenzi wa nyumba bora? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Joseph George Kakunda, maswali yake mawili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakapokuwa tumekamilisha sera ya nyumba na makazi jibu lako litakuwepo ndani yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye swali la pili; ni kwamba Wizara imeendelea kuandaa rasimu ya Taifa ya Nyumba ambayo pamoja na mambo mengine itatoa mwongozo wa viwango vya nyumba bora vinavyotakiwa kuzingatiwa na wadau wote. Aidha, sera hiyo itaweka uratibu rahisi wa upatikanaji wa vifaa vya ujenzi vya gharama nafuu, upatikanaji wa mikopo ya nyumba, mfumo wa uratibu wa wadau wa sekta ya nyumba na hivyo kuwezesha upatikanaji wa nyumba bora kuwa za gharama nafuu, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, mwaka 1973 Serikali ilifanya uamuzi wa kujenga Kiwanda cha Nguo cha Mbeya Textile cha pale Mbeya na lengo lilikuwa ni kwamba kiwanda hicho kitapata malighafi ya pamba kutoka katika Mikoa ya Shinyanga, Tabora na Mwanza kupitia barabara kutoka Tabora hadi Mbeya.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu barabara hiyo haijajengwa hadi leo, kiwanda kile kilikufa. Je, Serikali itajenga lini hiyo barabara kutoka Tabora hadi Mbeya hususan kipande cha kutoka Ipole hadi Rungwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya kutoka Ipole – Rungwa hadi Makongolosi ni barabara kuu na ni barabara ambayo ipo kwenye mpango na imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, kuanza kwa barabara hii kutategemea tu na fedha itakavyopatikana, lakini tayari ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuijenga barabara hii. Ahsante.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ninaomba niulize swali la nyongeza kwamba Wilaya ya Sikonge ambayo ni miongoni mwa Wilaya kubwa kieneo la kijiografia haina kituo chenye hadhi ya Kituo Kikuu cha Polisi cha Wilaya, badala yake wanatumia jengo dogo ambalo lilijengwa na chifu mwaka 1957. Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi chenye hadhi ya Kituo cha Polisi cha Wilaya? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Wilaya nyingi za polisi hazina majengo ya polisi ya ngazi ya Wilaya na ndio maana kama mnakumbuka Waheshimiwa Wabunge kwenye bajeti hii tumezungumzia haja ya kuanza kujenga vituo vya polisi ngazi ya Mkoa na Wilaya kule ambako vituo hivyo havipo. Sikonge najua ni eneo ambalo pia halina hadhi hiyo, kwa hiyo, tutaweka kipaumbele Mheshimiwa Mbunge ili katika mwaka ujao iweze kuzingatiwa katika bajeti tayari tuanze ujenzi wa kituo hicho. Nashukuru sana.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mimi katika Jimbo langu la Sikonge, wananchi pamoja na Mfuko wa Jimbo tumeshirikiana. Tuna maboma 14 ambayo yanahitaji milioni hamsini hamsini, jumla milioni 700 na halmashauri haina uwezo. Je, Serikali kuu haiwezi kutusaidia tuweze kumaliza maboma hayo 14.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Safari ni hatua, Serikali imeendelea kupeleka fedha katika Jimbo la Sikonge kwa ajili ya umalizaji wa maboma. Nimhakikishie kwamba tutaendelea kwa awamu kutafuta fedha ili kuendelea kukamilisha maboma haya. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mgogoro kati ya mpaka wa Mkoa wa Singida na Mkoa wa Tabora kwenye Wilaya za Uyui na Sikonge upo tangu mwaka 2002 na mwaka 2009 wataalamu walikubaliana kuchora upya huo mpaka. Sasa je, ni lini Serikali itaweka hizo beacons kutenganisha hii mipaka ya Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Singida ili kuondoa hiyo migogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Natumia fursa hii kuwaelekeza Wakuu wa Mikoa ya Tabora na Singida kuhakikisha wanatekeleza maelekezo ya Serikali ya kutatua migogoro ya mipaka kati ya wilaya na wilaya, lakini kati ya mkoa na mkoa ili wananchi waweze kufanya kazi kwa utulivu na amani.

Mheshimiwa Spika, tutafuatilia hilo kwa Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa hii miwili, nakuhakikishia kwamba Ofisi ya Rais TAMISEMI, itahakikisha beacons hizo zinawekwa na kuhakikisha kwamba wananchi wanatambua mipaka yao na kufanya kazi zao kwa amani. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na nipende kuishukuru sana Serikali kwa maelekezo ambayo imeshayatoa mpaka sasa hivi. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; tutarajie lini sasa hizi mbolea zilizofungashwa kwenye kilo 5, 10, 20 na 50 zitafika hasa madukani na kwa mawakala ili wananchi waweze kufaidika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; bei elekezi imekuwa inagusa zaidi mfuko wa kilo 50 wa mbolea; je, ni lini Serikali itatoa bei elekezi kwa kilo moja ya mbolea?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, lini mbolea hizi zitaanza kuonekana? Nataka tu nimtaarifu kwamba mbolea hizi tayari zimeshaanza kufungwa na Mkoa wa Tabora kwenye ghala kuu la Yara ni moja kati ya ghala ambalo linafunga mbolea hizi za kilo tano na hivi karibuni lilipata tatizo baada ya kugundua kwamba tulivyowapa nafasi ya kufunga mbolea za kilo tano/tano waliamua kufungasha vilevile na mbolea ambazo zimepitwa na wakati, tukalifunga ghala la Tabora na ghala la Iringa kwa sababu hiyo lakini makampuni tayari yameshaanza kufunga na kuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lini zitaanza kuuzwa kwa bei elekezi? Bei elekezi ya kilo 50 kama ni shilingi 75,000 maana yake mfungashaji yoyote anapofungasha kilo tano hatakiwi zile kilo tano/tano mifuko 10 thamani yake izidi kiwango cha shilingi 75,000 ya bei elekezi na tumeshachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichukua hatua kwa kampuni kwa Kampuni ya Minjingu tuliwagundua kwamba wanachukua mfuko wa kilo 50 wanafunga kilo tano/tano wanauza shilingi 13,000 maana yake ukijumlisha mifuko kumi ya kilo tano/tano inakuwa 130,000 tukawachukulia hatua na natumia Bunge lako Tukufu kuwaambia makampuni yote wasibadili msingi wa bei elekezi kama mbolea ni shilingi 75,000 kilo 50, maana yake ukifunga kilo 20 ni lazima thamani ya kilo 20 isizidi cost per unit ya kilo 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, natumia nafasi hii kuwaambia TFRA popote walipo wahakikishe wanafatilia ili wafanyabiashara wasi-take advantage katika jambo hili. Mwongozo wa bei utakaotangazwa hivi karibuni namwagiza Mkurugenzi wa TFRA kwamba tumekuwa na utaratibu wa kutoa bei elekezi ya kilo 50 sasa waweke na ujazo wa kilo tano, 10, 20 na 50. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali kwa majibu mazuri, nami nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza: Je, ni mikoa mingapi hapa nchini hadi sasa haijaunganishwa na Gridi ya Taifa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Nafahamu kwamba Kigoma nayo ipo katika mpango wa kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia vituo vya Urambo na Ipole Sikonge. Sasa swali ni kwamba wananchi watalipwa lini fidia kwenye ile njia ya kutoka Tabora kwenda Ipole?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na mikoa ambayo haijaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, mikoa miwili ya Katavi na Rukwa ndiyo ambayo haijaunganishwa kabisa kwenye Gridi ya Taifa. Mikoa ya Mtwara, Lindi, Kigoma na Kagera imeunganishwa kidogo kwa Msongo wa kilovolt 33, lakini miradi inaendelea ili tuiunganishe kwa Msongo Mkubwa wa Kilovolt 220 na Kilovolt 400. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na fidia ambayo ameuliza Mheshimiwa Mbunge, tayari tumeshafanyia kazi na tunategemea ifikapo tarehe 30 mwezi huu wa Novemba, 2023 wananchi wataanza kulipwa, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na nipende kuishukuru sana Serikali kwa maelekezo ambayo imeshayatoa mpaka sasa hivi. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; tutarajie lini sasa hizi mbolea zilizofungashwa kwenye kilo 5, 10, 20 na 50 zitafika hasa madukani na kwa mawakala ili wananchi waweze kufaidika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; bei elekezi imekuwa inagusa zaidi mfuko wa kilo 50 wa mbolea; je, ni lini Serikali itatoa bei elekezi kwa kilo moja ya mbolea?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, lini mbolea hizi zitaanza kuonekana? Nataka tu nimtaarifu kwamba mbolea hizi tayari zimeshaanza kufungwa na Mkoa wa Tabora kwenye ghala kuu la Yara ni moja kati ya ghala ambalo linafunga mbolea hizi za kilo tano na hivi karibuni lilipata tatizo baada ya kugundua kwamba tulivyowapa nafasi ya kufunga mbolea za kilo tano/tano waliamua kufungasha vilevile na mbolea ambazo zimepitwa na wakati, tukalifunga ghala la Tabora na ghala la Iringa kwa sababu hiyo lakini makampuni tayari yameshaanza kufunga na kuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lini zitaanza kuuzwa kwa bei elekezi? Bei elekezi ya kilo 50 kama ni shilingi 75,000 maana yake mfungashaji yoyote anapofungasha kilo tano hatakiwi zile kilo tano/tano mifuko 10 thamani yake izidi kiwango cha shilingi 75,000 ya bei elekezi na tumeshachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulichukua hatua kwa kampuni kwa Kampuni ya Minjingu tuliwagundua kwamba wanachukua mfuko wa kilo 50 wanafunga kilo tano/tano wanauza shilingi 13,000 maana yake ukijumlisha mifuko kumi ya kilo tano/tano inakuwa 130,000 tukawachukulia hatua na natumia Bunge lako Tukufu kuwaambia makampuni yote wasibadili msingi wa bei elekezi kama mbolea ni shilingi 75,000 kilo 50, maana yake ukifunga kilo 20 ni lazima thamani ya kilo 20 isizidi cost per unit ya kilo 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, natumia nafasi hii kuwaambia TFRA popote walipo wahakikishe wanafatilia ili wafanyabiashara wasi-take advantage katika jambo hili. Mwongozo wa bei utakaotangazwa hivi karibuni namwagiza Mkurugenzi wa TFRA kwamba tumekuwa na utaratibu wa kutoa bei elekezi ya kilo 50 sasa waweke na ujazo wa kilo tano, 10, 20 na 50. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana natambua kwamba kijiji ni mamlaka ya utawala, kata ni mamlaka ya utawala na halmashauri ya mji au ya wilaya au jiji ni mamlaka ya utawala. Nafahamu msimamo wa Serikali kuhusu uendeshwaji wa mamlaka za kiutawala. Sasa swali langu, jimbo siyo mamlaka ya utawala, Jimbo langu la Sikonge ili nifike kwenye tarafa ile ya mradi natembea kilometre 200, ili nifike kwenye Kata ya mbali kabisa mpakani mwa Singida natembea kilometre 400. Sasa swali langu ni kwamba kwa nini Serikali hairuhusu uanzishwaji wa majimbo mapya ili uwakilishi wa wananchi uwe mzuri zaidi hapa Bungeni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Kakunda Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli na ni sahihi kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema kuhusiana na mamlaka za utawala katika ngazi za vijiji, kata, halmashauri na maeneo mengine. Pili, jimbo ni eneo ambalo linauwakilishi wa wananchi na yeye ndiyo Mbunge wa jimbo hilo. Namshauri kwa sababu taratibu za kuomba majimbo mapya zinafahamika nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge afuate taratibu zile na kufikisha mahala ambapo kuna mamlaka hiyo hiyo ili waweze kuona uwezekano wa kuchukua hatua hizo kwa mujibu wa mahitaji ya jimbo lake, ahsante.