Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Joseph George Kakunda (165 total)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini hili tatizo la hizi kata limekuwa la muda mrefu na hasa ukizingatia kwamba kata zenyewe ziko pembezoni mwa Mji wa Musoma. Nataka kuuliza ni lini haya maji yatawafikia hizo kata kwa sababu wamekuwa na usumbufu wa muda mrefu?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, pamoja na matatizo ya mji wa Musoma pia kuna matatizo makubwa ya Mji wa Bunda na hasa Jimbo la Bunda ninakotoka mimi. Kuna kata saba zina matatizo makubwa ya uhaba wa maji ambazo ni Unyali, Kitale, Mgeta, Mihingo, Nyamaghunta na Salama; nilitaka kumuomba tu Waziri ni lini atafika? Nimuombe tu afike kwenye hizo kata saba za Jimbo langu ili aweze kujionea hali halisi ya uhaba wa maji katika jimbo hilo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni kweli kwamba, ni muda mrefu, lakini nimuahidi kwamba, mara mradi huu ambao umeanza kutekelezwa utakapokamilika wakazi hawa watafaidika na maji hayo. Swali la pili kuhusu Bunda; naomba nimuahidi Mheshimiwa Mwita Getere kwamba mara baada ya Mkutano huu wa Bunge nitatembelea Mkoa wa Mara na nitafika Bunda. Ahsante sana.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na niseme ninatambua jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano katika kuboresha elimu. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Je, Serikali ina mkakati gani katika mabweni haya 155 ambayo inatarajia kuyajenga katika mwaka wa fedha 2017/2018 kuhakikisha kwamba, inazingatia kipaumbele katika ujenzi wa mabweni katika shule zetu za kata?
La pili, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Mamlaka ya Elimu ya Juu Tanzania ambayo inaonekana inapata changamoto kutokana na kutokuwa na fedha za kutosha, inatengewa fedha za kutosha ili iweze kutekeleza majukumu yake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutekeleza mkakati wa kujenga mabweni kwa kushirikiana na Halmashuri na wananchi, kama ambavyo tumekuwa tukifanya na hivi natoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote kule kwenye maeneo yao ambako kuna ujenzi wa mabweni, basi wasaidie kuwahamasisha wananchi washiriki kikamilifu kwenye mkakati huu, lengo ni kuhakikisha kwamba, tunakamilisha ifikapo mwezi Juni mwakani, kama ambavyo tumejipanga.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tutaweka fungu maalum kwenye bajeti kwa ajili ya kuisaidia taasisi ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja pamoja na taasisi nyingine ambazo zinasaidia maendeleo ya elimu nchini. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pia nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Sasa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa ni sera na mpango wa Serikali kila wilaya kuwa na hospitali, je, ni lini ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro Vijijini utaanza licha ya jitihada nyingi za Serikali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Mvomero utakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) : Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba ni sera ya Serikali kujenga hospitali moja kila wilaya na napenda nimhakikishie Mheshimiwa Dokta Ishengoma na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali itaendelea kuwezesha ujenzi wa hospitali moja kila wilaya kwa awamu. Katika Mkoa wa Morogoro tumeanza na Manispaa ya Morogoro na tutaendelea na wilaya nyingine kwa awamu zinazofuata. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wangu, katika sehemu ya pili ya swali lake Mheshimiwa Dokta Ishengoma kuhusu Hospitali ya Mvomero na bahati nzuri tulikuwa pale Mvomero tukabaini baadhi ya upungufu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeshatenga fedha ya kumalizia jengo lile baada ya kuona upungufu ule na imani yangu ni kwamba kabla ya mwezi Januari hospitali ile itakuwa imekamilika ili wananchi wa Mvomero waweze kupata huduma vizuri. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Majimbo ya Longido na Ngorongoro ni majimbo ambayo yapo kwenye mazingira magumu sana na upatikanaji wa huduma za afya si wa uhakika. Wilaya ya Ngorongoro haina hospitali ya wilaya, Wilaya ya Longido imetengwa kwenye bajeti lakini utekelezaji bado. Je, ni lini Serikali itaweka mkazo kwenye majimbo haya ambayo kwa kweli yana mazingira magumu ya kijiografia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema mwenyewe kwamba Majimbo ya Longido na Ngorongoro yapo katika mazingira magumu na Wilaya ya Longido hakuna hospitali na Wilaya ya Ngorongoro tayari iko katika bajeti. Naomba ushirikiano wake mara fedha ambazo zipo kwenye bajeti zitakapopelekwa, ashiriki kikamilifu katika kusimamia ili matumizi ya fedha zile yawe mazuri kama ambavyo ilikusudiwa. Mwaka ujao wa fedha tushirikiane naye kuhakikisha kwamba Longido nao tunawawekea bajeti. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tabora Manispaa tuna tatizo kubwa la msongamano wa wagonjwa katika Hospitali Teule ya Kitete na kwa kuzingatia hilo, Tabora Halmashauri kwa kushirikiana na Madiwani pamoja na wananchi wengine tumetenga eneo kwa ajili ya kujengwa Hospitali ya Wilaya ambayo mpaka sasa hivi ujenzi wake unasuasua kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Je, Serikali inajipanga vipi katika kusaidia uwezeshaji wa kuweza kujenga hospitali hiyo ya wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimshukuru Mheshimiwa Mwakasaka pamoja na Waheshimiwa Madiwani katika Manispaa ya Tabora kwa kutenga eneo la kujenga Hospitali mpya kwenye Manispaa ya Tabora ambayo itakuwa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huohuo, kwa kuzingatia kwamba Hospitali ya Kitete ni kweli imezidiwa na mzigo maana yake ndiyo hospitali pekee ya rufaa ya mkoa, Serikali inaahidi na namwomba ushirikiano wake, wakati tutakapokuwa tunaweka kwenye bajeti tushirikiane ili tuweze kupitisha kwa pamoja. Ahsante sana.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wananchi wa Kijiji cha Mtisi wanapata shida sana, hawana kabisa eneo la kilimo. Nafikiri umeona kabisa hapa jinsi gani eneo la hifadhi ni kubwa zaidi kuliko eneo la kilimo na kaya zimeonekana hapa. Naishukuru Serikali imepanga kuwapa ardhi Novemba mwishoni lakini wananchi wa Mtisi wanahitaji kulima sasa, sasa hivi ndiyo kipindi cha maandalizi ya kilimo, wanatakiwa waandae mashamba yao. Je, Serikali haioni ni vema kubadilisha hii Novemba mwishoni wafanye Novemba hii mwanzoni ili wananchi wale waweze kupata maeneo ya kilimo waweze kupata chakula ndani ya familia zao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, ndani ya Kata hii ya Sitalike kwenye Vijiji vya Matandalani na Igongwe kutokana na ardhi ndogo wako ndani ya ramani toka 1972, lakini Serikali ilienda kuwabomolea nyumba zao na mpaka leo hii imekuwa tafrani, wala hawaelewi hatma ya maisha yao. Je, Serikali ina mpango gani na wananchi wa Matandalani na Igongwe? Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kwenda kwenye Kata ya Sitalike kuona adha hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kurejea majibu yangu ya swali la msingi katika kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Anna Lupembe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimesema kwamba ifikapo mwishoni lakini hadi sasa kazi za kuwapatia ardhi wananchi hao zinaendelea. Hadi jana kaya 200 zilikuwa zimeshatambuliwa na zilikuwa zimeshatengewa eneo maalum. Kwa hiyo, bado zoezi hilo linaendelea ile mwishoni mwa Novemba ni kumalizia kazi, kazi itakuwa imekamilika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili amesema kwamba wananchi wa Kijiji cha Matandalani na Igongwe walibomolewa nyumba ni kwa sababu walikuwa kwenye hifadhi. Natoa wito kwa wananchi ambao wako kwenye maeneo ya hifadhi kwamba wanatakiwa waondoke wenyewe badala ya kusubiri kuondolewa kwa nguvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa shida hiyo iliyopo kule Matandalani na Igongwe na Halmashauri ya Nsimbo kwa ujumla, nilipita juzi lakini niko tayari kwenda tena kama matatizo yataendelea kuzidi kuwepo.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Mkoa wa Katavi ni kimbilio la wananchi wengi ambao wamekosa ardhi ya kilimo na wakati huohuo ardhi iliyopo Mkoa wa Katavi asilimia themanini imemilikiwa na misitu ya Serikali kiasi kwamba wananchi walio wengi wamekosa kupata nafasi ya kufanya shughuli zao za kiuchumi kupitia sekta ya kilimo hasa katika kata za Sibwesa, Kasekese, Katuma, Bulamata ambako kuna migogoro mingi ya ardhi. Je, Serikali imejipanga vipi kutatua kero ya ukosefu wa ardhi ili wananchi waweze kuitumia ipasavyo kujikwamua kiuchumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyozungumza katika Mkoa wa Katavi sehemu kubwa ya ardhi ni misitu na maeneo ya hifadhi. Ni lengo la Serikali kuendeleza maeneo hayo katika msingi wa kuendeleza misitu na hifadhi kwa ajili ya ustawi wa mazingira lakini vilevile kwa ajili ya kuendeleza ile hali nzuri ya hewa ikiwemo mvua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba katika halmashauri na vijiji vyote tuendelee kuhakikisha kwamba kila kijiji kinakuwa na mpango ardhi wa eneo lake ambao unaainisha maeneo ya kulima, maeneo ya kuishi kama kijiji, maeneo ya mifugo na malisho ili kusudi tuwe na mipango endelevu ya maisha yetu. Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ndilo jibu langu.
MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Wilaya ya Siha kwenye Kata Ngarenairobi na Ndumeti wananchi hawana maeneo ya kulima pamoja na makazi, wamekaa kwenye mabonde wakati wamezungukwa na heka zaidi ya elfu hamsini na sita za Serikali lakini kukiwepo na mashamba makubwa sana ya ushirika ndani ya Wilaya ya Siha ambayo hayatumiki kama inavyotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumwomba Waziri kama atakuwa tayari kufuatana na mimi baada ya Bunge hili tukatizame mazingira ya Wilaya ya Siha na huko Ndumeti pamoja Ngarenairobi na maeneo mengine tuweze kuamua namna ya kupanga hiyo ardhi kubwa sana iliyoko Siha kwa matumizi ya wananchi kwa ajili ya kilimo, makazi lakini vilevile kutenga maeneo ya viwanda na uwekezaji mwingine kwa ajli ya Serikali na sera iliyopo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa la Siha na maeneo kama hayo ni uwekezaji mkubwa ambao unafanywa na wananchi wachache. Kwa hiyo, tungependa tupate kwanza mpango wa Halmashauri yake halafu ndiyo tuweze kuufanyia kazi. Ahsante sana.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Mheshimiwa Waziri anasema ujenzi unaweza kuanza mwaka 2018/2019, unaweza kuanza. Sasa wananchi wa Mji wa Ujiji na Kasulu kwa ujumla wanataka kupata uhakika, yaani ile commitment ya uhakika kwamba utaanza 2018 au unaweza maana ukisema unaweza, unaweza usianze.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Mji wa Mugumu tulipewa kilomita mbili mwaka wa fedha uliopita lakini kilomita mbili hizi tumetangaza mara tatu hazijapata mkandarasi kwa sababu ya kilometa chache. Je, Wizara iko tayari kwa mwaka ujao wa fedha kutuongezea kilomita iwe rahisi kwa ajili ya wakandarasi kufanya mobilization?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumesema kwamba ujenzi unaweza ukaanza kwa sababu bajeti haijapitishwa na Bunge. Naomba Mheshimiwa Mbunge tushirikiane naye kupitisha kwanza bajeti ndiyo ujenzi uweze kufanyika vinginevyo kama Bunge halitapitisha bajeti hiyo, ujenzi hauwezi kuanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili amesema kwamba wamepata ugumu kupata mkandarasi kwa sababu ya ufupi wa barabara ya kilomita. Ningemwomba Mheshimiwa Mbunge amshauri Mkurugenzi wake wa Halmashauri aweze kutembelea Halmashauri za jirani ambazo zimeweza kujenga hizo hizo kilomita mbili na zimepata wakandarasi. Ahsante sana.
MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, ili hawa watumishi wa Serikali za Mitaa waweze kutoa huduma kwa ufanisi wanahitaji kupata mafunzo ya mara kwa mara ili kuboresha utendaji wao. Kwa kuwa kwa muda mrefu mafunzo yamesimamishwa, tunategemeaje hawa watumishi waweze kutoa huduma ipasavyo? Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, viongozi ambao wako karibu sana wananchi ni Watendaji wa Kata na Mitaa pamoja na Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Kata, ndio wapo karibu sana na wananchi na ndio ambao wanatoa huduma karibu kabisa na wananchi. Watendaji wanapata mshahara lakini Wenyeviti hawapati chochote. Je, Serikali ina mpango gani kwa ajili ya kuwamotisha Wenyeviti ili waweze kutoa huduma vizuri kwa wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, katika maeneo ambayo yamejengewa uwezo kwa hali ya juu kabisa ni hili eneo la Serikali za Mitaa. Kuna programu nyingi sana za kisekta zimeendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa nyakatii mbalimbali. Kuna Programu kwa mfano ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo, Programu ya Kuendeleza Sekta ya Maji, zote hizi zimekuwa na mafunzo mbalimbali kwa watendaji wa Serikali za mitaa kwa ajili ya kuimarisha uwezo wao, hasa hasa zile kada za fedha, ununuzi na wahandisi. Serikali inatoa commitment ya kuendelea kutoa mafunzo mara fedha zinapopatikana.
Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu posho za Wenyeviti wa Serikali za Vijiji na Vitongoji. Mwongozo uliopo ni kwamba kila Halmashauri inatakiwa iboreshe makusanyo yake ya ndani, iongeze makusanyo yake ya ndani na mwongozo uliopo ni kwamba asilimia 20 ya mapato yake ya ndani yanatakiwa yatumike kwa ajili ya posho na agizo ambalo limetolewa na kusisitizwa na Serikali ni kwamba wale ambao wanachelewesha kulipa posho za wenyeviti wa vijiji na vitongoji sasa itabidi wachukuliwe hatua.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa wananchi wa Wilaya ya Kakonko kwa sasa wanapata huduma katika Kituo cha Afya cha Kakonko na kituo hicho kimezidiwa kwa sababu msongamano wa watu ni mkubwa. Kituo hicho kinahudumia wananchi kutoka hadi Mkoa jirani wa Kagera kwa maana ya wananchi wa Nyakanazi, Kalenge pia na wakimbizi kwa sababu katika Wilaya ile kuna kambi za wakimbizi, Waziri amesema kwamba mwaka 2017/2018 zimetengwa shilingi milioni 500.
Je, Waziri yupo tayari sasa kutokana na jinsi wananchi wanavyopata shida pamoja na waganga na wauguzi kwa sababu watu wakiwa wengi waganga nao wanachanganyikiwa, yupo tayari kufuatilia hizo shilingi milioni 500 ziweze kwenda mara moja Kakonko kwenda kuwasaidia wananchi? (Makofi)
Swali la pili; kwa wakati huu ambapo Wilaya ya Uvinza haina Hospitali ya Wilaya, wananchi wanapata huduma katika vituo vya afya na zahanati, lakini vituo hivyo vya afya pamoja na zahanati havina watumishi wa kutosha.
Je, katika mgao huu wa wafanyakazi ambao wataajiriwa kwa sasa, Serikali iko tayari kabisa kupeleka watumishi wengi wa kutosha kwenda kusaidia katika Wilaya ya Uvinza ambayo haina Hospitali ya Wilaya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Genzabuke kwa jinsi ambavyo anafuatilia huduma hasa kwa wanawake katika Mkoa wa Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, napenda kumthibitishia kwamba fedha hizo ambazo zimetengwa kwenye bajeti ya 2017/2018 nitazifuatilia na kuzisimimamia mimi mwenyewe binafsi kuhakikisha kwamba zimekwenda haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili, wiki hii iliyopita tumekamilisha upatikanaji wa watumishi 2,008 ambao sasa hivi wanaendelea kugawanywa katika Halmashauri mbalimbali. Leo hii nitahakikisha kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza imepata watumishi wa kutosha angalau kwa mahitaji ya asilimia 50. (Makofi)
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Sera ya Elimu Bure imewasaidia baadhi ya wazazi wasio na uwezo kuandikisha watoto shuleni, lakini wakati huo huo bado kuna michango kadhaa inayoendelea kwa baadhi ya shule na michango hii imerudisha nyuma morali ya wazazi kuchangia kwa juhudi katika maendeleo mbalimbali ya shule.
Je, Serikali ipo tayari sasa kutoa elimu kwa wananchi kwamba sera ni elimu bila ada na siyo elimu bure ili kuwafanya wananchi waweze kuchangia kwa nguvu kama ilivyokuwa zamani? (Makofi)
Swali la pili, shule za Sekondari za Keni, Shimbi na Bustani katika Halmashauri ya Wilaya ya Rombo ni shule ambazo zimejengwa kwa mtindo wa ghorofa kwa sababu ya uhaba wa ardhi katika Wilaya ya Rombo na sasa zina muda karibu wa zaidi ya miaka 10 wananchi wameshindwa kuzikamilisha.
Je, Serikali ipo tayari katika bajeti ijayo katika bajeti
ijayo kuzipokea hizi shule na kuzikamilisha ili kuweza kuunga mkono nguvu za wananchi katika jitihada zao za kufanya maendeleo mengine kama kumalizia maabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS – TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubalina na Mheshimiwa Selasini kwamba kuna michango ambayo inaruhusiwa. Lakini michango ile ina utaratibu kwamba ili kusudi mchango uweze kukubalika kisheria ni lazima Kamati ya Shule au bodi ya shule iwe imeujadili na kupeleka kwa wadau ambao ni wazazi, wakipitisha wanaomba kibali kwa Mkuu wa Mkoa, wakipata kibali basi hapo wanaweza wakaendelea na kuchangishana. Huo ni utaratibu ambao ni mzuri, namshauri Mheshimiwa Mbunge autumie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa swali lake
la pili, sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Wizara ya Elimu tupo tayari kukaa na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kujadili namna ambavyo tunaweza tukaboresha utaratibu wa kuzikamilisha hizi shule ambazo anazizungumzia. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naomba niulize swali dogo la nyongeza.
Hivi karibuni Naibu Waziri wa Elimu ametoa kauli akisema watoto wakitaka kuolewa wawe na cheti cha kumaliza form four, wakati huo huo Serikali ilisema wale wanafunzi ambao wanapata ujauzito wakiwa shuleni wasiendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningependa nipate
kauli ya Serikali katika mkanganyiko huu, nini hasa ni kauli ya Serikali sahihi. Vipi wanafunzi ambao wanapata mimba wakiwa shuleni na hawaendelei kwa mfumo wa shule, lakini na kauli ya Waziri ya kusema anayetaka kuolewa awe na cheti cha form four? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS – TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI) -MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa majibu sahihi kwa Mheshimiwa Waitara pamoja na Watanzania wote waliopata mkanganyiko kuhusu kauli hiyo ni kwamba, nilisema Sera Mpya ya Elimu ya mwaka 2014 huko tunakoelekea inabadilisha mfumo wa sasa wa elimu kwenda kwenye mfumo mpya ambao utahitaji mtoto aanze chekechea mwaka mmoja, asome shule ya msingi miaka sita, shule ya sekondari miaka minne na hii itakuwa ni lazima kwa yeyote atakayeanza darasa la kwanza hadi amalize form four. Kwa hiyo, nikasema kwamba tutakapofika wakati huo, kithibitisho muhimu kwamba huyu mtoto sasa amemaliza form four ni school leaving certificate, wakati huo siyo leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndugu yangu Mheshimiwa Waitara huo ni ufafanuzi sahihi kabisa wa sera mpya. Sasa hivi tunaandaa utaratibu na maandalizi ikiwepo pamoja na miundombinu ili tuweze hatimae kuitekeleza hiyo sera muda utakapofika. Kwa hiyo, usiwe na mkanganyiko ndugu yangu Waitara. (Makofi)
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mzuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna tatizo limejitokeza, kuna Waraka unasema walimu wa arts ambao wamezidi katika shule za sekondari wanahamishiwa shule za msingi. Huu uhamisho unakuwaje ilhali Rais wetu alisema walimu wasihamishwe mpaka pale fungu lao litakapopatikana.
Je, hao walimu wameshaandaliwa mafao yao ya uhamisho ili waende kwenye vituo vyao vipya huku tayari Wizara imeshasema mpaka itakapofikia tarehe 15 Februari walimu hawa wawe wamefika vituoni kwao? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, napenda kujua, huu uhamisho wa kuwatoa walimu wa arts kutoka sekondari kuwapeleka primary unaweza kuathiri ufundishaji wa wanafunzi wa huko primary. Je, Serikali imeandaa induction course kwa ajili ya walimu hawa ili waweze ku-coup na ufundishaji wa walimu wa primary? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): MheshimiwaMwenyekiti, swali la kwanza kwa wale wanaohusika ambao wamepata Waraka Rasmi wakiusoma vizuri watagundua kwamba maelekezo yaliyomo katika Waraka ule ni kwamba uhamisho unafanyika kutoka kwenye shule ya sekondari kwenda kwenye shule ya msingi ambayo iko karibu na eneo hilo, siyo kumtoa kwenye Wilaya moja kumpeleka Wilaya nyingine. Uhamisho ule ni wa ndani ya kata kwa hiyo hauna gharama za uhamisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ule uhamisho kutoka shule za sekondari kwenda primary umezingatia kwanza kipaumbele kwa wale walimu ambao walijiendeleza, zamani walikuwa walimu wa shule ya msingi wakajiendeleza wakapata diploma na degree hatimaye wakahamishiwa katika shule za sekondari.
Kwa hiyo, kuwarejesha kwenye shule za msingi ambazo wana uzoefu nazo hakuhitaji induction course ya aina yoyote. Kwa hiyo, hicho ndiyo kipaumbele ambacho kimewekwa na kimezingatia walimu wa diploma na walimu wa degree ya kwanza. Ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nitoe masikitiko makubwa sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, ambapo tarehe 8 Juni, 2016 niliuliza swali kuhusu vijiji na kata hizo hizo na aliyekuwa Naibu Waziri na sasa ni Waziri mwenye dhamana TAMISEMI alinipa majibu ambayo yalikuwa yanaeleza kwamba vijiji hivyo vimetengewa bajeti ya shilingi milioni 49.5 ambayo itatekelezwa mwaka 2016/2017. Mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea, ni Bunge hili hili ambalo linatoa majibu hayo na leo tena nimepewa asilimia hiyohiyo 49.5 kwamba itatekelezwa 2018/2019. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali langu, ni lini Serikali itapeleka pesa kwa wananchi hawa, toka mwaka 1995 mpaka leo ni upembuzi yakinifu unafanyika, ni lini hawa wananchi watapata maji? (Makofi)
MheshimiwaMwenyekiti, swali la pili, ni kwa nini hawakufanya upembuzi wa kina wakati bajeti ilitengwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, ni kweli kwamba usanifu wa kina haukufanyika ule wa zamani, lakini kwa sasa tunatarajia usanifu kina utafanyika mwaka 2018/2019 kwa ajili ya utekelezaji wa kumaliza kabisa matatizo ya maji kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ambalo lilikuwa ndiyo la kwanza, ni kwamba kazi ambazo zimefanyika kuanzia 2016 mpaka Desemba, 2017 nimesema hapa kwamba tumejenga visima sita katika Kata za Magulilwa, Luhota, Maboga na Mgama. Hii kazi imefanyika na taarifa hizi zimetoka kule kule kwenye Halmashauri yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, taarifa za kina zaidi namuomba sana tushirikiane naye baada ya kikao hiki ili tuweze kushauriana vizuri namna bora ya kuhakikisha kwamba tunamaliza matatizo ya wananchi kwenye maeneo hayo.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Kakunda, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kumekuwa na malalamiko mengi sana kwa Wakazi wa Dodoma wakiwemo Wabunge na Taasisi mbalimbali za Kiserikali kwamba ili waweze kupata huduma ya ardhi Manispaa ya Dodoma, basi kuna mzunguko mkubwa sana na mlolongo mkubwa sana.
Je, Serikali ipo tayari hivi sasa kufanya uchunguzi maalum na kuchukua hatua kwa kuwa, sasa Manispaa ya Dodoma ni Mji Mkuu kwamba tunahitaji huduma hizi ziende kwa haraka? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, zipo Taasisi za Serikali ambazo zinahamia Dodoma hivi sasa, zinataka kujenga ofisi zao hapa Dodoma, lakini bado kumekuwa na urasimu mkubwa sana taasisi hizo kupewa ardhi pale Manispaa.
Je, Serikali ipo tayari hivi sasa kuweka utaratibu maalum ili Taasisi hizi za Kiserikali ama Taasisi za Umma ziweze kupewa maeneo ya kuweza kujenga ofisi zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma na ndiyo maana wakazi wa Kusini wanamwita mashine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mlundikano wa kazi uliokuwepo katika kipindi hiki cha awali cha utekelezaji wa majukumu mapya ya kuunganisha majukumu ya iliyokuwa Manispaa ya Dodoma na ile iliyokuwa CDA ndio umefanya kuwe na baadhi ya malalmiko katika hatua za awali za utekelezaji wa kazi, kwa sababu kulikuwa na migogoro mingi sana ya viwanja, mahitaji ya kubadilisha mikataba mingi sana na hapo hapo kuna mahitaji ya kuendelea kupima maeneo mapya. Kwa hiyo, haya matatizo ambayo Mheshimiwa Maftaha ameyataja ni matatizo ya mpito tu ambayo yatarekebishwa hivi karibuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali lake la pili, hadi sasa Manispaa imepima viwanja 1,288 na ambavyo tayari hati zake zimetayarishwa. Maeneo ambayo ni Mji Maalum wa Serikali yamepimwa viwanja 147, ikiwemo Ikulu, Wizara zote zimepatiwa hati na vilevile taasisi za umma na viwanja vya mabalozi 64.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nakuonesha hati ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI ni hii hapa, tayari imepatikana na ipo Ofisini. Wizara zote zina hati kama hii. Taasisi zote za umma ambazo zinahitaji ardhi, waende Manispaa pale watapewa hati zao ambazo zitawawezesha kupata maeneo ya kuweza kujenga ofisi zao haraka sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika maeneo ya Nala wamepima viwanja 922 na kiwanja cha michezo cha Nzuguni kimepimwa, kile ambacho tulipata msaada kutoka Morocco na viwanja 218 katika maeneo mengine.
Waheshimwa Wabunge na wananchi kwa ujumla wanakaribishwa waombe viwanja Manispaa na mimi kama msimamizi wa Manispaa hiyo, nawaahidi kwamba watakuwa wamepata hati kabla ya mwisho wa mwezi huu wa pili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo limepimwa viwanja vya Serikali ni hili hapa na naweza nikalionyesha Waheshimiwa Wabunge waweze kuliona. Kazi imefanyika vizuri. (Makofi)
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Dodoma sasa hivi ni Makao Makuu ya nchi na Manispaa wameongezewa jukumu lingine la ardhi ambalo lilikuwa la CDA, lakini kuna upungufu mkubwa wa vitendea kazi pale Manispaa hasa ile Idara ya Ardhi pamoja na watendaji ni wachache kiasi kwamba ukienda pale bado kuna watu wengi wanakaa kwenye foleni kwa muda mrefu.
Serikali sasa kwa kutambua kwamba Dodoma ni Makao Makuu, imejipangaje kuhakikisha kwamba Manispaa ya Dodoma inawezeshwa kwa vitendea kazi, miundombinu pamoja na watendaji wa kutosha ili wafanye kazi kwa weledi na kwa haraka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupata nguvu kazi ya kutosha kutoka kwenye ile iliyokuwa CDA, ni kweli kwamba bado kuna mahitaji ya watumishi na baadhi ya vitendea kazi na hivyo vinafanyiwa kazi mpaka mwezi wa sita, matatizo mengi yatakuwa yamekamilika.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Matatizo ya maji yaliyoko Bukoba Vijijini yanafanana na matatizo tuliyonayo kule Karatu. Kata ya Rotia na Kata ya Mang’ola zina upungufu mkubwa wa maji kutokana na miundombinu iliyokuwepo kuwa ya muda mrefu na hivyo kushindwa kupeleka huduma ya maji stahiki. Je, ni lini sasa Serikali itatenga fedha ili kuboresha huduma ya maji katika Kata hizo mbili. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) : Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo yeye mwenyewe amekiri maeneo ya Karatu ni miongoni mwa maeneo ambayo tangu zamani kumekuwa na uwekezaji kwenye miradi ya maji na ndiyo maana miradi hiyo aliyoitaja amesema kwamba miradi ile ina uchakavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye awamu ya pili ya utekelezaji wa program ya maji tumeweka kipaumbele kikubwa kwanza kukarabati miradi iliyokuwepo ikiwemo hiyo ya Kata ya Rotya na Kata na Mang’ola ambayo kuna miundombinu ya maji ya muda mrefu. Kwa hiyo kipaumbele ni kukarabati kwanza hiyo kabla hatujaanza miradi mipya.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nitakuwa nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Serikali imejipanga kuhakikisha wanafikisha umeme pamoja na maji hasa zaidi kwenye shule pamoja na sehemu zingine za kutolea huduma za kijamii, lakini ningependa kwa uhakika kabisa aseme kwamba ni lini Serikali itatimiza suala hili kwa sababu ni muda mrefu wamekuwa wakiliongea kila mara bila kuwa na tarehe ya uhakika kwamba itakapofika wakati fulani tutakuwa kwa kweli tumetekeleza, bado shule nyingi pamoja na vituo vya afya vinakosa huduma ya umeme pamoja na maji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna vijiji vingi sana, kama anavyosema kwamba Serikali imeazimia kupeleka umeme kwenye vijiji vyote zaidi ya 7,000, lakini ukipita Jimbo la Ndanda kwa mfano Vijiji vya Nangoo, Liputu, Ndolo pamoja na Mdenga vinapitiwa na umeme wa msongo wa megawati 33. Sasa Waziri angetusaidia kutueleza ni lini kwa hakika Serikali sasa wako tayari kushusha umeme ule kwa ajili ya matumizi ya watu wale walioko chini ya hizi waya ambazo kwao ni hatari kwa maisha?Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa
Mwenyekiti, katika maswali yake mawili ya nyongeza aliyouliza Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda yeye mwenyewe ni shahidi anafahamu kwa sababu ameshiriki kupitisha bajeti hapa anajua mipango ya Serikali ilivyo. Sina shaka kwamba anatambua kwamba ahadi iliyoko kwenye Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano inaendelea kutekelezwa vizuri na tuna uhakika vijiji vyote nilivyovitaja kwenye jibu la msingi vitapata umeme pamoja na vitongoji vyake kama ambavyo Wizara ya Nishati imeahidi, na mikakati iko wazi na yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge ni shahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la maji, Mheshimiwa Waziri wa Maji ametoa ahadi hapa Bungeni kuhusu kutekeleza awamu ya pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, na hii itaongezeka kasi zaidi pale ambapo tutaanza kutekeleza miradi ya maji vijijini kupitia ile Wakala wa Maji Vijijini ambao utafanya kazi sawasawa na REA inavyofanya kazi. Kwa hiyo, ndugu yangu Mwambe ondoa shaka katika swali lako la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, huu umeme ambao umepita kwenye vijiji alivyovitaja na msongo anaujua ameutaja, mimi kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati namuahidi kwamba mikakati ya Serikali itatekelezwa na wanavijiji aliowataja hao watapata umeme.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa madaraka ya Wakuu wa Mikoa ambayo ipo kisheria si kushusha vyeo walimu ambao wamekuwa wakifundisha watoto wetu katika mazingira magumu. Hata hivyo hili limekuwa likijitokeza sasa baadhi ya Wakuu wa Mikoa akiwemo Mkuu wangu wa Mkoa wa Manyara kuwashusha vyeo walimu kwa kisingizo cha kwamba eti wamefelisha wakati watoto wanafeli kwa sababu ya mazingira magumu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nifahamu nini tamko la Serikali juu ya Wakuu hao wa Mikoa akiwemo wa Mkoa wa Manyara ambaye ameshusha Simanjiro, Kiteto na Babati Vijijini na anaendelea na ziara kuendelea kuwashusha walimu vyeo, nini kauli ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo inaeleweka ni kwamba Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya ndio wasimamizi wakuu wa shughuli zote za Serikali katika Wilaya na Mikoa yao. Kwa hiyo, kama inatokea masuala yanayohusu uzembe au utoro wanayo mamlaka ya kutoa maelekezo kwa mamlaka za nidhamu ambazo ni TSC. Mamlaka ya nidhamu TSC inaanzia katika eneo la shule, shuleni pale Mwalimu Mkuu mwenyewe ni mwakilishi wa TSC. Kwa hiyo, kama yeye mwenye ndio anakuwa anaongoza katika kuonyesha uzembe labda na utoro, hiyo lazima hatua ziweze kuchukuliwa. Lakini mambo mengine ambayo pengine yanaonesha kwamba labda kuna mambo ambayo yamevuka mpaka, tutayafanyia uchunguzi maalumu, ahsante sana.
MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Pamoja na tatizo la malimbikizo ya mishahara ya walimu na kupandishwa madaraja bila kurekebishiwa mishahara yao kuna tatizo kubwa la walimu la muda mrefu ambalo ni ahadi ya Serikali karibu miaka sita sasa kwamba walimu wangepewa posho ya kufundishia yaani teaching allowance. Ni mara kadhaa Serikali imekua na kigugumizi hapa Bungeni na imekuwa haina jibu. Madaraja hayo au teaching allowance hiyo wamekuwa wakipewa Wakuu wa Shule na Waratibu wa Elimu tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuiuliza, je, Serikali ina mkakati gani wa ziada kuhakikisha kwamba ahadi waliyoiweka mwaka 2012 kwamba watawapatia walimu posho ya kufundishia (teaching allowance) sasa itakuwa imepatiwa ufumbuzi wa kudumu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inajipanga kwa mambo mengi na ahadi zetu ni nyingi ambazo bado tunaendelea kuzitekeleza na hii ahadi ambayo anaisema Mheshimiwa Mbunge, nayo tutaitekeleza mara tutakapokuwa vizuri kifedha.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kueleza masikitiko yangu kuhusiana na mradi huu, mwaka 2014 alikuja Katibu Mkuu wa Chama akadanganywa kuhusu mradi huu. Akaja Waziri Kamwelwe Januari mwaka jana akadanganywa kuhusu mradi huu, mimi nimekuja Ofisi na hao uliowasema mwaka jana Desemba mradi ulikuwa uishe tukadanganywa tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, nahitaji muda gani na mara ngapi kuja hapa kuuliza maswali haya na uwongo wa kudanganywa namna hii, wananchi kule umetaja 17,000 hawana maji?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa miradi ya maji katika Jimbo la Mbulu Vijijini iko mingi, nayo hakuna muda ambao umetajwa wa kumalizika na mikataba imeisha, na mimi kule sina fundi kabisa au Mhandisi wa Maji ndani ya Halmashauri yangu.
Je, unanisaidia pamoja na kwamba tutakaa baadae kuhusu ya watumishi katika Wizara hii au katika sekta ya maji?
MHE. JOSEPH J. KAKUNDA - NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (TAMISEMI):
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema wakati ninajibu swali la msingi kwamba mradi huu kimsingi umeshatekelezwa kwa asilimia 90 bado asilimia 10 tu, zikazuka changamoto ambazo zilizungumzwa kwenye kikao, zikaonekana kwamba zinatatulika, lakini usiku wa leo nimepata mwendelezo unaohusu changamoto za ziada ambazo tunahitaji kuzitatua baada tu ya kikao hiki.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wote wa Haydom na Jimbo la Mbulu Vijijini kwamba mradi huu kama tutatatua hizi changamoto ambazo amekumbana nazo mkandarasi ninaamini ndani ya wiki mbili hadi tatu hii asilimia 10 itakuwa imekamilishwa, ndiyo maana tumesema ifikapo mwezi Aprili, tutakuwa tumekamilisha mradi huu.
Swali la pili, kuhusu watumishi, napenda nimwakikishie ndugu yangu Mheshimiwa Flatei kwamba tunaiangalia Wilaya ya Mbulu kwa ujumla na Halmashauri yake ya Mbulu Vijijini kwa uangalifu mkubwa kutokana na mazingira ya eneo lenyewe na physiology ya eneo lenyewe la Wilaya ambalo nimefika ni juu na tambarare zimechanganyika na kwa hiyo tutampatia Mhandisi wa Maji hivi karibuni.(Makofi)
MHE. GODFREY W. MGIMWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nitakuwa na swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Halmashauri nyingi zimekuwa hazitengi fedha hizi kwa ajili ya vijana na akina mama; lakini vile vile tuna tatizo sasa hivi ambalo tungekuwa makini zaidi kuliangalia suala la ndugu zetu walemavu, kwamba kuweze kuwa na uwezekano sasa wa kuzitenga fedha kutoka katika hizi asilimia 10 kwa ajili ya walemavu, vijana na akina mama.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa sababu majibu ya msingi yameshatolewa ningependa kufahamu kwa hizi Halmashauri ambazo kwa ujumla zimeshindwa kutenga fedha hizi kwa ajili ya vijana kama mimi akina mama; na kama tulivyoongea kuhusu walemavu ningependa kufahamu sasa.
Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba inazibana halmashauri hizi ili ziweze kupata mapato ya ndani kwa uhakika na kuhakikisha kwamba inatenga fedha hizi kwa ajili ya makundi haya? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali la nyongeza ambalo linawagusa akina mama na vijana nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kupitia Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ameshatoa waraka tangu mwaka jana mwezi wa saba kuelekeza Halmashauri zote nchini kuhakikisha kwamba wanatenga asilimia 10 kwa ajili ya mikopo ya vijana na wanawake na hilo ndiyo maana nimesema hapa kupitia Bunge lako Tukufu kwamba ni lazima watenge na wasipotenga sasa Serikali itaanza kuchukua hatua za kiutumishi dhidi ya Wakurugenzi ambao hawatengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kwa sababu kinachotakiwa kufanyika ni kutenga kile ambacho kimekusanywa, kama kimekusanywa bilioni 10 basi asilimia 10 ya bilioni 10 lazima itengwe kwa ajili ya wanawake na vijana. (Makofi)
MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Na mimi naomba kuuliza swali la nyongeza kuwa hili suala la kutenga asilimia 10 wa ajili ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu linaonekana kama halijakaa kisheria sana na ndiyo maana wakati mwingine wanatumia hiyo loopholes za kuepuka kutenga hilo fungu.
Je, Serikali ina mkakati wowote wa kuhakikisha kuwa sheria au kanuni zinarekebishwa ili kuhakikisha kuwa hili jambo linakuwa kisheria zaidi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nilijulishe Bunge lako Tukufu kwamba tumeshapokea maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu pendekezo la kupitia upya sheria ambayo ndiyo tunaiangalia ambayo ilikuwa ndio misingi wa kuanzishwa hii mifuko ili tuweze kuona kwamba tunaweza kurekebisha sehemu gani ili kuweze kuzibana zaidi Halmashauri kuhusu kutenga asilimia 10.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa fedha hizi zimeleta mgogoro sana zinapowekwa kwenye akaunti ya pamoja, je, Serikali haioni haja sasa kuzielekeza Halmashauri kuanzisha akaunti maalum kwa ajili ya hii asilimia 10 peke yake? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuliahidi Bunge lako Tukufu kwamba tumechukua maoni ya Mheshimiwa Sima ambayo naamini ni maoni ya Waheshimiwa Wabunge wote na tutalifanyia kazi.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa vipo vikundi vya akina mama ambavyo vimeanzishwa na kuunda SACCOS, lakini halmashauri hawatoi pesa hiyo asilimia 10 kuvipatia vikundi hivyo na wakati vikundi hivyo havijaweza kukopeshwa na mabenki au taasisi mbalimbali za kifedha.Je, ni kwa nini sasa Serikali isiagize Halmashauri ili vikundi hivyo navyo vilivyoundwa kama SACCOS viweze kukopeshwa pesa hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Genzambuke kwa kuzidi kuvijali vikundi vya SACCOS ambavyo vimeanzishwa kwenye Halmashauri nyingi hapa nchini ikiwemo Halmashauri ya Kasulu pale anakotoka.
Hili suala ni wazo zuri na mimi naomba sana sana badala ya kulijibu hapa haraka haraka tulichukue tukalifanyie kazi zaidi kwa sababu malengo Mfuko wa Vijana na Wanawake ni kukopesha wale vijana ambao wanajishughulisha na kazi za uzalishaji mali moja kwa moja. Sasa hili suala la kusema kwamba tuwakopeshe halafu na wao wakopeshane ni wazo jipya ambalo linahitaji kujadiliwa zaidi kitaalam ili tuweze kutoa maelekezo. Ahsante sana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WALEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri sana yaliyotolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba tu niliarifu tu Bunge lako Tukufu kwamba pamoja na kuendelea kulifanyia kazi jambo hili naomba kuendelea kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge kuwa katika kutoa mikopo kwa vijana kupitia Mfuko wa Vijana wa asilimia tano, zile zinazotengeneza asilimia 10 kwenye Halmashauri tayari Serikali ilishagiza vijana kupitia halmashauri zao waunde SACCOS za vijana ili waweze kunufaika na mikopo hiyo na kupitia kwenye hizo SACCOS waweze kujikopesha na mikopo hiyo iwe revolving. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo pamoja na vijana ni lazima pia kuwaangalia na akina mama. Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na hasa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi limeanza kuweka mkakati maalum wa kuhakikisha linafikia vikundi vya VICOBA na SACCOS za wanawake na vijana katika nchi nzima ya Tanzania. Nimuombe sana Mheshimiwa Genzabuke, kwa kuwa kupitia Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi tuna mifuko takribani 17 ya kuwawezesha wananchi Mheshimiwa Genzabuke awasiliane na mimi tuwaelekeze akina mama hawa wa Kigoma wanaweza wakasaidiwaje. (Makofi)
MHE. ESTER A. MAHAWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa ruzuku hii iliyotajwa hapa kila Halmashauri imejipangia namna gani itatumia hizo ruzuku na hakuna uniformity katika matumizi hayo, na kama ambavyo tulimaliza suala la upungufu wa madawati na maabara nchini, je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kutoa maagizo makali kidogo ili kumaliza suala hili la upungufu wa vyoo mashuleni?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; wanaoteseka sana katika suala zima la upungufu wa vyoo nchini ni hasa mabinti walioko kwenye shule za sekondari. Kila mtu anafahamu wanapokuwa kwenye mzunguko ule kidogo wanapata taabu kulingana na ukosefu wa vyoo tena vyenye maji safi.
Je, ni lini sasa hususani katika Mkoa wetu wa Manyara Serikali itachukua hatua ya kumaliza tatizo hili hasa katika shule ya Komoto na Bagara Sekondari pale Babati Mjini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Ester Mahawe kwa swali la msingi pamoja na maswali yake ya nyongeza. Ni changamoto kubwa sana ambayo tunakabiliana nayo na yeye mwenyewe ni shahidi manake ni mdau katika sekta ya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama alivyozungumza tumekuwa na mikakati mbalimbali kuhusu miundombinu mbalimbali hususani maabara na madarasa. Lakini kwa wakati huu ambao bado tunahangaika kumalizia ujenzi wa maabara hususani kumalizia maboma ya maabara na kuzipatia vifaa, na bado wananchi wanaendelea kuchangia; mimi nilikuwa namuomba Mheshimiwa Mahawe aungane na sisi kwamba tutoe kwanza kipaumbele kwenye hizi fedha ambazo zimetengwa ili kusudi tuone zitafikia hatua gani wakati huo huo tunamalizia suala la maabara ili baadaye tuweze kuchukua hatua zaidi kama anavyopendekeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuhusu miundombinu ya maji katika shule zetu. Tumeshatoa maelekezo kwamba kila shule inapopanga ujenzi wa madarasa ni muhimu sana wakazingatia kuweka miundombinu ya kuvuna maji ya mvua. Hiyo ni miundombinu ambayo ni ya gharama nafuu badala ya kuwa na miradi ya maji ya kutumia vyanzo vingine ambavyo vinatumia fedha nyingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hilo ni agizo lilishatolewa na maelekezo yalishatolewa. Inatakiwa sasa Wakurugenzi wa halmashauri zote pale ambapo shule inajengwa lazima kuwe na miundombinu ya maji ya mvua, ikiwa ni pamoja na shule ambazo amezitaja, baada tu ya kikao cha leo nitafuatilia kule Halmashauri ya Babati ili kusudi tuweze kujua hizo shule Mkurugenzi ana mpango gani kuzipatia huduma za maji. Ahsante sana.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa miundombinu hiyo katika vyoo kwenye shule zetu za msingi na sekondari bado haizingatii mahitaji ya watoto wenye ulemavu; na baadhi ya watoto wenye ulemavu wanalazimika kutambaa katika vyoo hivyo ambavyo wakati mwingine ni vichafu na vinahatarisha afya kwa watoto wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nashukuru kwa majibu yake, lakini sijasikia hata yeye mwenyewe kuona kwa jicho la pili uhitaji wa watoto hawa wenye mahitaji maalum katika vyoo hivi. Ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba wanazingatia mahitaji ya watoto wenye ulemavu ili na wao waweze kusoma vizuri? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Amina Mollel kwa kufuatilia hasa hasa masuala yanayowahusu wanafunzi wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba michoro ya zamani ilikuwa na upungufu wa kutozingatia mahitaji ya watoto au wanafunzi wenye ulemavu. Hata hivyo michoro ambayo ilipitishwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mwaka jana yote imezingatia kwamba darasa, choo na bweni na miundombinu mingine ya shule ambayo inatumiwa na wanafunzi lazima izingatie mahitaji ya watoto wenye ulemavu, na ushahidi ni mabweni mapya na madarasa mapya na vyoo vipya ambavyo vimejengwa tangu mwaka jana mwezi wa saba vyote vimezingatia mahitaji hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Amina Mollel kwenda kufanya ukaguzi kwenye maeneo yote ambayo hatimaye tutaelekeza wafanye marekebisho, ahsante sana.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa niipongeze sana Serikali kwa mkakati huu mzuri ambao umeiuweka na kwa sehemu imetekeleza lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile moja kati ya migogoro ambayo inatokana na tatizo hili ambalo limeelezwa ni migogoro kati ya wakulima na wafugaji. Na kwa vile migogoro hii kwa sehemu kubwa inachangiwa na ukosefu wa mipango bora ya matumizi ya ardhi kwa baadhi ya maeneo, na kwa vile pamoja na jitihada nzuri za Serikali migogoro hii imechangiwa na Halmashauri za wilaya hasa watumishi ambao hawapo tayari kwenda kufanya kazi hii bila kulipwa posho, sasa je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba vijiji vyote ambavyo havina mpango bora wa ardhi vipatiwe mpango huo? Na pili ina mpango gani kuhakikisha kwamba watumishi ambao hawapo tayari kwenda kufanya kazi hizi bila kupata posho wanachukuliwa hatua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama kwa kuijali sana hii sekta ambayo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu, hata viwanda vinategemea sana sekta ya kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu vijiji ambavyo hadi sasa havina mipango ya matumizi bora ya ardhi tunayo changamoto kubwa sana, moja, ili kijiji kipime, kiwe na mpango wa matumizi bora ya ardhi yake bajeti ambayo inahitajika angalau kuweza kuwezesha upimaji huo inaanzia kati ya shilingi milioni tano hadi milioni nane na baadhi ya vijiji ambavyo ni vikubwa hadi milioni kumi. Sasa kwa sababu Halmashauri nyingi bado hazijawa na uwezo wa kuwa na fedha hizo utekelezaji umekuwa ni wa pole pole sana, ikiwemo Halmashauri yake ya Madaba hadi sasa ni vijiji nane tu ndio vina mipango ya matumizi bora ya ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninatoa wito kwa vijiji ambavyo vina fedha, vipo vijiji ambavyo vina fedha, vigharamie mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa manufaa ya kiuchumi ya wananchi wa vijiji hivyo. Wakurugenzi wa halmashauri zote nchini wafanye mapitio ya vijiji vyote na kuvishauri vile ambavyo vina uwezo wa kugharamia zoezi hilo viweze kugharamia, na vile ambavyo havina kabisa uwezo halmashauri ijipange kugharamia.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunawachukulia hatua gani watumishi ambao hawataki kwenda kufanya kazi vijijini hadi walipwe posho. Nataka nitoe angalizo kwao, kwamba walipoajiriwa walipewa maeneo ya kufanya kazi. Kama mtu amepewa eneo la kijiji halafu ndani ya kijiji hataki kufanya kazi mpaka alipwe posho huyu mtu tunatakiwa tupate taarifa zake mapema iwezekanavyo ili tuweze kumchukulia hatua na Wakurugenzi wa Halmashauri waanze kuchukua hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshatoa maagizo wale watumishi ambao wana mazoea ya kukaa Makao Makuu ya Halmashauri bila kwenda kutembelea vijiji waanze kupangiwa kazi na Wakurugenzi wa Halmashauri bila kujali kama kuna posho au hakuna, ili mradi tu aweze kuwezeshwa vyombo vya usafiri vya kuweza kuwafikisha kwenye vijiji wanavyotakiwa kwenda kufanya kazi, basi. Kwa hiyo, hiyo ndio ushauri wangu na maelekezo yangu kupitia Bunge lako Tukufu.

NAIBU WAZIRI WA ARDHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru sana Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa majibu yake mazuri kulingana na swali lililoulizwa juu ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi. Wizara imejipanga vizuri katika mwaka wa fedha unaokuja kwa ajili ya kupima maeneo ambayo yana migogoro mingi, hasa yale maeneo yanayozunguka kwenye mbuga za wanyama. Tayari ile Tume ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi imeshaingia makubaliano pia na wenzetu wa TANAPA, kwa hiyo kuna vijiji vingi ambavyo vitapimwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo tukumbuke tu kwamba mpango wa kupanga matumizi bora ya ardhi au masuala ya mpango miji ni jukumu la Halmashauri zenyewe husika. Kama alivyosema Naibu Waziri bado pia vijiji na maeneo ambayo yanakuwa na pesa wanayo fursa hiyo. Kama Wizara tuna-facilitate uwezekano wa kuweza kuwapa elimu na namna bora ya kupima, lakini Wizara tumejipanga vizuri na tutakwenda kupunguza sana kero hii. Kwa hiyo, tunachowaomba sana wananchi tuwe tayari katika suala hilo.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba niongezee na niliarifu Bunge lako tukufu kwamba Wizara ya Kilimo tumeandaa mpango mkakati wa kilimo ASDP II ambao utahusisha zaidi ya Wizara sita. Hata hivyo kutokana na swali la msingi ni kwamba katika hizi green house tumepanga kila halmashauri iweze kuwa na green house ili wananchi waweze kujifunza, kwa sababu hizo green house ambazo tunazizungumzia zinachukua eneo dogo lakini uzalishaji wake unakuwa ni mkubwa zaidi na vile vile ni katika kuendeleza hii tasnia yetu ya horticulture.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni kwamba Wizara tunatoa mafunzo na maelekezo ambayo yanafanyika kwa kutumia udongo na teknolojia mbalimbali za kuhifadhi udongo huo ili kuzuia mmomonyoko na vile vile kuweza kuongeza tija kwa ajili ya kupunguza tatizo hili nililolisema, ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza:
Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kabisa yanaonyesha jinsi ambavyo walimu wetu wamekuwa wakikosa nyumba za kuishi, walimu wa sekondari 52,000 hawana mahala pa kuishi na walimu 130,300 wa shule za msingi hawana nyumba za kuishi. Tumesema tunataka kuwa na elimu bora katika nchi yetu na hatufahamu walimu wanaishi wapi.
Je, Serikali sasa haioni ni wakati muafaka sasa wa kuamuru Jeshi la Polisi liweze kujenga nyumba hizi za walimu kama walivyofanya kwa Mererani kuzuia ile migodi yetu, tatizo hili ili liweze kuisha kwa haraka?
Swali la pili, walimu wamekuwa wakikosa udhamini katika mabenki mbalimbali kwa kutokuwa na mali za kudhaminiwa na taasisi alizozitaja Mheshimiwa Naibu Waziri ni hizo ambazo huwezi kudhaminiwa kama huna dhamana ya vitu visivyohamishika kama viwanja, magari na vitu vingine na tunatambua hali za walimu wetu zilivyo.
Je, sasa Serikali haioni haja kwamba ni wakati muafaka Mifuko ya Hifadhi ya Jamii iweze kuwa dhamana kwa walimu wetu wakati bado wakiwa kazini na siyo baada ya kustaafu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nisisitize kwamba katika jibu langu la msingi ile takwimu niliyoitaja kwa faida ya Bunge lako tukufu haikumaanisha kwamba walimu hao hawana makazi kabisa. Nimesema kwamba walimu hao wanaishi katika aidha, nyumba za kupanga au nyumba zao binafsi, hilo ndilo jibu langu la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya kwanza ya swali lake kwamba kwa nini Serikali isiamuru Jeshi la Polisi kujenga nyumba za walimu nchi nzima, hilo ninaomba sana majeshi yetu yana kazi zake maalum ambayo yamepewa kufanya na waliojenga ukuta wa Mererani siyo Jeshi la Polisi ni Kitengo cha Ujenzi cha Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Tumekuwa tukiwapa kazi nyingi sana, SUMA JKT kujenga nyumba za walimu kujenga nyumba za walimu katika mahali pengi. Hata kwake kule Iringa tumewapa sehemu nyingi tu SUMA JKT kujenga nyumba na tutaendelea kuwapa mikataba ya kujenga nyumba.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema kwamba ujenzi wa nyumba ambao unafanywa na Serikali utaendelea kuwa kidogo kidogo kwa sababu unategemea sana bajeti ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, napenda nimuondoe wasiwasi kuhusu dhamana. Karibu mabenki yote na taasisi zote zinazokopesha hakuna dhamana zaidi ya mshahara wa mtumishi. Kinachotakiwa tu ni kwamba mtumishi asiwe anadaiwa mikopo mingine hilo ndiyo jambo la msingi, kama mtumishi hadaiwi mikopo mingine anao uwezo wa kukopa na ataamua mwenyewe, je, akope kwa kurejesha miaka mitatu au akope kwa kurejesha miaka 10 au akope kwa kurejesha miaka 25 ni yeye mwenyewe katika makubaliano ya fomu yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kuwasisitiza watumishi wote nchi nzima na Wakurugenzi wa Halmashauri ambao wako chini yangu nataka niwaambie kwamba mikopo hiyo ya watumishi ipo, waingie makubaliano maalum na hizo taasisi na mabenki ili kusudi watumishi waweze kukopesha waweze kujenga nyumba zao binafsi. (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa maendeleo ya Taifa lolote lile yanatokana na mifumo yake ya elimu inayojali utu wa binadamu; na kwa kuwa Walimu ni sehemu muhimu sana katika uzalishaji wa maendeleo endelevu katika Taifa letu.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kutenga fungu maalum la fedha hata kama ni kukopa ili kuondoa kero hizi katika sekta ya elimu ikiweko nyumba za walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbatia ambaye ni mkereketwa mkubwa sana wa sekta ya elimu napenda nimhakikishie kwamba mawazo yake ni sawa tu na mawazo ya Serikali. Hivi karibuni tumekamilisha kukokotoa gharama zinazohitajika kuweza kukamilisha miundombinu inayohitajika katika sekta ya elimu ili tuanze utekelezaji kwa asilimia 100 wa Sera yetu ya Taifa ya Elimu ya mwaka 2014, hilo analoliongea ni mojawapo ya yale ambayo tumeyaingiza katika hizo gharama na gharama za awali katika rasimu inaonyesha wazi kwamba tunahitaji takribani trilioni 13 ili kuweza kukamilisha miundombinu yote inayohitajika.
Naomba Mheshimiwa Mbatia na Bunge lako Tukufu liweze kuwa na subira, tutakapokamilisha tutafanya majadiliano maalum ili tuweze kupata fedha zinazohitajika kwa sekta ya elimu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwanza ningependa kutambua kazi inayofanyika kwenye Kata ya Mwena, Chikundi pamoja na Chigugu ya kusambaza miundombinu kwa ajili ya maji na Mheshimiwa Waziri wa Maji ametoa ushirikiano mkubwa pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, bwawa hili la Lukuledi tunalolitaja hapa sasa hivi kwa mara ya kwanza kabisa lilichimbwa mwaka 1955 lakini mpaka sasa hivi limekauka zaidi ya mara tano kwa sababu linategemea tu maji ya mvua kutokana na mabadiliko ya tabianchi.
Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kuiongezea nguvu Mamlaka ya Maji Safi Masasi (MANAWASA) kwa kazi nzuri inayofanywa na Engineer David ili waweze kufikisha maji Kata ya Lukuledi na vijiji vyake vyote maji safi na salama badala ya kuendelea na huo mradi wa bwawa?
Swali la pili, pamoja na nia njema kabisa ya Serikali kutaka kuweka mabwawa kwenye maeneo waliyoyataja hapo ya Chingulungulu, Mihima pamoja na Mpanyani lakini tu niseme wanachokisema hapa sasa hivi, mwaka huu wametenga kazi ya usanifu.
Je, nini nia ya Serikali kuhakikisha wanawaondolea wananchi hawa taabu ya kupata maji kwa siku zijazo kwa sababu bajeti ya mwaka huu inaonesha tu ni kazi ya usanifu peke yake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya kwanza ya swali lake ni kweli kwamba bwawa hili limekuwa linapata matatizo makubwa ya kukauka kwa sababu mbalimbali, lakini miongoni mwa sababu hizo ni kujaa mchanga na matatizo mengine yanayosababishwa na kutotunza mazingira.
Mheshimiwa Naibu Spika, wazo lake kwamba tuwaambie MANAWASA wapeleke maji katika maeneo hayo badala ya kutegemea bwawa lile, naomba sana nimshauri tusubiri usanifu wa kina ukamilike, usanifu huo utatushauri kama chanzo hicho kitatosheleza mahitaji ya maeneo hayo na kama usanifu huo utashauri kwamba chanzo hicho hakitatosheleza basi tutaona njia nyingine ya kupata chanzo kingine ikiwemo hiyo ya kuchukua maji kutoka kwenye chanzo kilecha Mbwinji ambacho ndiyo kinategemewa na MANAWASA, kwa sasa hivi naomba sana tusimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutachukua maji kutoka Mbwinji.
Mheshimiwa Naibu Spika, wito wangu kwenye sehemu hii ya swali la kwanza, ninamuomba sana usanifu utakapokamilika, kama utakaposhauri kwamba wananchi watunze mazingira na wengine watapisha katika eneo la mita 500 kutoka kwenye chanzo kwa ajili ya utunzaji wa mazingira ya bwawa basi naomba sana ashiriki kuwaelimisha wananchi wakubali hatua hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili ya swali ameonesha wasiwasi kwamba mwaka huu tuna bajeti ya kufanya usanifu peke yake, ndiyo tumetenga shilingi milioni 60 ili tufanye usanifu wa kina na ukamilike na DDCA wamepewa hiyo kazi wakamilishe usanifu mwaka huu wa 2017/2018. Watakapotupatia gharama sasa hapo ndiyo tutapanga lini utekelezaji utaanza kwa kushirikiana na Wizara ya Maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, namuondolea wasiwasi kwamba suala hili kwa sababu sasa limeletwa katika utaratibu wa vipaumbele, asiwe na wasiwasi awahakikishie wananchi kwamba tutatekeleza mradi huu ndani ya mwaka mmoja.(Makofi)
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba sasa niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, shule za kata tangu zimeanzishwa sasa takribani ni muongo mmoja; na kwa bahati mimi nilikuwa ni miongoni mwa walimu walioanzisha shule za kata. Matatizo na changamoto yaliyokuwepo mwaka 2006/2007 wakati shule za kata zinaanzishwa kama vile madarasa, ukosefu wa maabara, ukosefu wa walimu wa sayansi na hisabati, bado mpaka leo changamoto zile zipo.
Naomba sasa kujua ni lini Serikali itatuhakikishia kwamba changamoto za walimu wa sayansi, hisabati na madarasa katika shule zetu zitakwisha? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hivi karibuni Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati anazindua Mbio za Mwenge kule Geita, aliorodhesha mikoa inayoongoza kwa utoro na Mkoa wa Lindi siyo miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa utoro; bahati mbaya ni miongoni mwa mikoa inayofanya vibaya sana katika matokeo ya kidato cha nne na matokeo ya darasa la saba. Moja ya mkakati wa Mkoa ni kuhakikisha tunatoa chakula mashuleni.
Naomba sasa leo Serikali iji-commit hapa; je, iko tayari sasa kutuhakikishia kwamba sisi wa Mkoa wa Lindi tuendelee na programu ya kuwashirikisha wazazi ili waendelee kuchangia chakula ili matokeo yaweze kuboreka katika shule zetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, hadi sasa kuanzia mwezi Oktoba, 2017 hadi sasa tumeajiri walimu 200 wa masomo ya sayansi na hisabati. Mpango uliopo hadi tarehe 30 Juni tutaajiri walimu 6,000 na lengo tunataka kuondoa kabisa tatizo la walimu wa sayansi na hisabati katika shule za sekondari ifikapo mwaka 2020, maana yake inakwenda polepole.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la miundombinu pamoja na chakula, nimhakikishie Mheshimiwa Hamidu Bobali na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali haijakataza michango ya wananchi kuchangia miundombinu ya shule zikiwemo maabara. Kilichokatazwa ni kumpa adhabu mwanafunzi ya kukosa masomo kwa sababu tu mzazi wake hajatoa mchango. Kwa hiyo, hiyo ndiyo iliyokatazwa, lakini kupitia Serikali za Vijiji, mnaruhusiwa kuendelea kuhamasisha wananchi ili wachangie maendeleo ya shule zao ikiwemo miundombinu pamoja na chakula. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, wamesema wanaajiri walimu wa sayansi, hisabati na kadhalika, lakini bado tatizo la walimu hao ni kubwa. Nataka kujua tu, wamefanya sensa, ni walimu wangapi wa sayansi ambao kila siku wanaacha kazi kwa sababu ya maslahi duni katika Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili ni gumu sana, kwa sababu hatuna takwimu za kila mwaka kwamba ni walimu wangapi wa sayansi na hisabati wanaacha kazi.
Lakini comfort niliyonayo na ambayo nataka niwape Waheshimiwa Wabunge ni kwamba malalamiko tuliyonayo ni ya walimu kutaka kuhama haraka katika shule wanazopelekwa, yaani mwalimu anaweza akapelekwa kwenye shule fulani, akikaa baada ya wiki mbili anataka ahame. Hiyo ndiyo changamoto kubwa tuliyonayo ambayo tunaishughulikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuacha kazi, hilo naomba sana tutoe majibu baadae.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maelezo yake Mheshimiwa Waziri amekiri kabisa kuwa kuna upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi. Pamoja na mikakati mizuri ambayo Wizara mnaifanya, mtambue kabisa kwamba walimu wetu wa sayansi wana work load kubwa sana uki- compare na walimu wengine. Tuna shule moja Wilaya ya Kilolo inaitwa Shule ya Lukosi ina mwalimu mmoja wa sayansi kati ya watoto 700.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu kwa Mheshimiwa Waziri; ni incentives gani kama Wizara imejipanga kuhakikisha inawapa motisha hata hawa walimu wachache waliopo ili wawe chachu kwa watoto wetu waweze kufanya vizuri? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri ambalo ameonesha concern kubwa kuhusu walimu wa sayansi, namna ambavyo tunaweza tukawafanya wajisikie kwamba Serikali inawajali.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo tumefanya kama Serikali, ni kuhakikisha kwamba tumeweka package ambayo ni nzuri zaidi kwa walimu wa sayansi hata wanapoanza kazi kuliko hata walimu wa sanaa. Kwa hiyo, hiyo ni sehemu ya motisha kwao.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunasisitiza sana kwamba wanapofika katika shule, Walimu Wakuu na Maafisa Elimu wawapokee vizuri, wawape counseling ili wakubali kuishi katika maeneo wanayopelekwa, hilo ndiyo jambo la msingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mengine tutaendelea kuboresha kwa sababu mengine hatuwezi kuweka motisha kubwa sana, kwa sababu nao ni watumishi sawasawa na watumishi wengine. Sasa kama utabagua, una watumishi ambao ni walimu halafu unabagua; huyu lazima apewe nyumba, huyu kwa sababu una uhasama naye, asipewe nyumba. Hicho nadhani itakuwa ni kitu ambacho siyo kizuri sana katika Taifa letu.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la nyongeza ni kama ifuatavyo; mwaka 2016 tulipata tatizo kule Lindi kwenye shule ya sekondari ambayo ni shule kongwe. Wananchi wamejitahidi kadri walivyoweza lakini bajeti yake ni shilingi bilioni mbili. Serikali itatusaidiaje juu ya ujenzi wa shule hiyo ambayo iliungua moto mwaka 2016? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Salma Kikwete kwa sababu amekuwa akijitolea sana kuhusu kuinua elimu katika Mkoa wa Lindi, na hasa hii shule ya sekondari ya Lindi, ameichukua imekuwa kipaumbele kikubwa sana kwake. Kwa kweli namshukuru sana, ameongoza harambee nyingi, hata juzi tulikuwa kwenye harambee pale Dar es Salaam kwa ajili ya kuichangia hii shule na tukapata karibu shilingi milioni 282; na mwaka 2018 ilifanyika harambee zikapatikana shilingi milioni 550. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Salma Kikwete na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Lindi na wananchi wa Lindi kwa ujumla kwamba shule hii ambayo iliungua madarasa tisa na ofisi tatu za Walimu mwaka 2016, mwaka ujao wa fedha tutahakikisha kwamba madarasa 27 na ofisi tisa za walimu ambazo wamepanga kujenga yatakamilika. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante. Pia namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Sheria Namba Tisa ya Mwaka 2010 inamzungumzia mtoto mwenye ulemavu kupata haki ya elimu pamoja na kulindwa. Watoto hawa wenye usonji, kama nilivyosema kwenye swali langu la msingi wana mazingira tete. Sasa je, nili lini, au je, upi ni mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba watoto hawa wanapata elimu toshelezi katika mazingira yao ya miundombinu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, watoto wenye usonji kwa kawaida wanatakiwa kila watoto watano wawe na Mwalimu mmoja. Sasa katika majibu ya msingi tunaambiwa watoto wapo 1,416 na Walimu wapo 157, maana yake watoto hawa wanatiwa wawe na Walimu wasiopungua 283. Sasa je, ni lini Walimu hawa watapewa elimu stahiki ili waweze kuwapa watoto wenye ulemavu, hasa usonji elimu inayostahiki? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Mama Salma Kikwete, yeye ni mdau mkubwa wa elimu na kwa kweli hasa katika elimu maalum ametoa mchango mkubwa sana wa mawazo kuhusu kuendeleza watoto hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wenye usonji mara nyingi huzaliwa kawaida na usonji huanza kuonekana baada ya mwaka mmoja na nusu hadi miaka miwili. Kwa hiyo, wazazi wengi wamekuwa wakipata shida ya kuwatambua vizuri kwamba huyu mtoto ana usonji, kwa hiyo, imekuwa vigumu hata kuwaratibu. Matokeo yake wengine wamekuwa labda wakiwapiga wanadhani ni watukutu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inao mpango maalum wa kwanza kuwatambua watoto hao wote na kuwasajili ili hatimaye tuhakikishe kwamba wote wanapata elimu kama ilivyo haki ya kila mtoto Mtanzania kupata elimu. kwa hiyo, mkakati wetu tutaanza zoezi la kuwatambua na kuwasajili ili hatimaye wapate elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, nakubaliana naye kwamba katika kila watoto watano wanatakiwa kuwa na Mwalimu mmoja lakini standard ambayo ni nzuri sana ya Kimataifa inatakiwa anapomfundisha amfundishe akiwa peke yake (one to one), hiyo ndiyo standard ya kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, upungufu wa walimu waliopo sasa hivi wanaofundisha shuleni ni mkubwa kama alivyoainisha. Hata hivyo, kwa kuwa tunao Walimu wengine ambao wameshapata mafunzo hayo kule Patandi halafu bado hawajahamishiwa kwenye hizo shule ambazo zinafundisha watoto hawa kwa sasa, ndiyo maana nimetoa agizo kwamba ifikapo Desemba wawe wamehamishiwa kwenye hizi shule ili kusudi watoto hawa waweze kupata haki yao ya msingi kabisa ya elimu.
MHE. SUSAN A.LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwamba kuna tatizo kubwa la upungufu wa Walimu hawa, lakini nina taarifa kwamba tuna Walimu wengi sana waliosoma katika vyuo kwa mfano Chuo cha Tabora cha Viziwi, wamesomea kufundisha watoto hawa, lakini wapo mitaani na wana resources.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni kwa nini Serikali isiwachukue Walimu hawa ambao wamesomea kwa miaka mitatu degree zao na kuendelea kuchukua Walimu ambao wamepata kozi za juu juu tu za mafunzo kazini wakati tunajua tuna tatizo kubwa sana la Walimu kwa ajili ya watoto hawa wenye ulemavu mbalimbali pamoja na viziwi na hawa wengine wa usonji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Susan Lyimo kwa sababu kwanza amekuwa ananiletea maswali mengi hata kwenye karatasi, vi-note na nimekuwa nikimpa maelezo ya kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili namuahidi katika Walimu ambao tutawaajiri hivi karibuni, kipaumbele kitakuwa ni kwa hawa ambao wana taaluma ya elimu maalum ambao hawajaajiriwa ili waajiriwe haraka waweze kutusaidia katika shughuli zetu.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, ni kweli majibu hayo aliyotoa Mheshimiwa Naibu Waziri ni ya kweli kabisa kwa hatua ambazo zinaendelea katika Halmashauri, lakini huyu Mkandarasi Maswi kimsingi amekuwa akitusumbua sasa muda mrefu kweli amekuwa akitoa sababu mbalimbali kwamba sijui ni masika hawezi kutafuta haya maji. Sasa naomba kwa sababu ilikuwa ni commitment ya Waziri wa Maji alifika katika Kata hii na katika kijiji hiki, je, Wizara hii pamoja na Wizara ya Maji wanaweza wakatupa ushirikiano DDCA wakatusaidia, kwa sababu wao wanafahamu ni wapi maji yanapatikana badala ya huyu Maswi akaendelea kutusumbua na wananchi wale wakapata maji?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, nakubaliana na Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba huyu Mkandarasi wa awali anayechimba maji katika Kijiji cha Imbilili kwa kweli amekuwa akitusumbua sana, lakini hayo tutayafanyia kazi kwenye Baraza letu kama alivyoshauri. Naomba nifahamu Wizara iko tayari sasa kuangalia bili tunazolipa za maji katika Mji wetu wa Babati kwa sababu wananchi wetu wakilalamika sana, pamoja na upungufu wa maji lakini wanatozwa bili kubwa sana za maji. Je, Wizara hii na Wizara ya Maji mko tayari ku-review bili ambazo wananchi wa Babati wanalipa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kitaalam ni kweli kwamba huwezi kufanya utafiti mpya wa maji chini ya ardhi hasa kama unataka kuchimba visima wakati huu wa masika. Kwa hiyo, kama Mkandarasi ameomba muda kidogo apewe ambapo yupo asilimia 25 kwa sasa hivi, kama anapewa muda wa mwezi wa Tano anaweza akachukua muda wa mwezi mmoja kumalizia visima vile ambavyo alikuwa anachimba kwenye vile vijiji na ikiwezekana mwezi wa Sita au mwezi wa Saba akamaliza kazi ya kuchimba visima. Nashauri kitaalam apewe muda wa mwezi wa Tano na Sita ili kusudi aweze kukamilisha kazi yake vizuri.
Mheshimiwa Spika, kama Mkandarasi huyu Maswi ataondolewa sasa hivi halafu wakaanza mchakato mpya wa kumpata kazi mtu mwingine wanaweza wakachukua miezi sita kukamilisha kumpata Mkandarasi ambayo itakuwa ni siyo faida sana kwa wananchi. Kwa hiyo, nashauri avumiliwe kidogo kwa kipindi hiki cha miezi miwili ama mitatu ili aweze kukamilisha kazi yake. Wizarani tutasukuma ili kusudi aweze kufanya kazi yake kitaalam zaidi.
Mheshimiwa Spika, swali la pili, ningependa kuisifu sana Mamlaka ya Maji Mjini Babati, kama ambavyo imesifiwa pale ambapo Waziri Mkuu alienda mwaka juzi waliisifu wao wenyewe BUWASA kwamba inafanya kazi nzuri na hata Mheshimiwa Diwani Sumaye ambaye anatoka kwenye Kata ile ya Sigino ambako hakuna maji kabisa, mbele ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema kwamba bwana kwa kweli tunashukuru wenzetu wa Mjini Babati wanapata maji vizuri, tatizo hapo ni bili.
Mheshimiwa Spika, ili kusudi ianzishwe bili, EWURA kabla hawajaidhinisha huwa wanafanya kitu kinaitwa mkutano wa wadau, wanajadili, wakishakubaliana wadau ndiyo bili ile inaidhinishwa. Kwa hiyo, nashauri Halmashauri kama inaona kwamba bili ni kubwa basi wawasiliane na EWURA kwa barua rasmi ili kusudi suala hilo liweze kutatuliwa. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri ambaye na yeye pia ni mkazi wa Mkoa wa Tabora katika Jimbo la Sikonge anafahamu hali halisi ya elimu za watoto wetu na ndugu zetu katika mkoa wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea hapa na takwimu zinazooneshwa ni shule chache ambazo zimefaulu kwa kiwango kikubwa zinatengenezewa takwimu na zinaonekana kwamba ndiyo takwimu halisi; lakini uhalisia uliopo katika Mkoa wa Tabora, elimu yetu imeshuka kutokana na miundombinu hakuna walimu. …

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha wa kuboresha miundombinu ya elimu katika Mkoa wa Tabora ili watoto wetu waweze kufanya vizuri?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika shule za sekondari ambazo ni shule zilizokuwa zinafaulisha vizuri miaka ya nyuma ambapo watu wengi humu ndani wamesoma katika shule hizo leo shule hizo zimekuwa na changamoto za vitanda, changamoto za viti na changamoto za miundombinu mbalimbali. Serikali ina mpango gani pia wa kuweza kuhakikisha maeneo yale yanaboreshwa ili shule zile ziweze kufanyavizuri kama ilivyokuwa hapo awali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimsifu san binamu yangu kwa kufuatailia sana sekta ya elimu. Nakubaliana nae kwamba kuna baadhi ya shule hususani za pembezoni kabisa hazifanyi vizuri lakini mara nyingi tunapozungumzia mkoa huwa tunajumlisha kupata matokeo ya kimkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, Serikali ina mpango gani kuboresha miundombinu? Kama tulivyowasilisha bajeti yetu vizuri ya juzi, tumejidhatiti kweli kweli. Mwaka huu tumepeleka walimu 112 katika shule za msingi, walimu wa sayansi tumepeleka walimu 20 katika Mkoa wa Tabora lakini kwa mwakani 2018/2019 tutajenga vyumba vya madarasa 207, matundu ya vyoo 689, nyumba za walimu 123 na kwa upande wa sekondari tutajenga nyumba za walimu 179, vyumba vya madarasa 159, matundu ya vyoo 166 na kukamilisha maabara 163 kwa ajili ya masomo ya sayansi. Tunaamini kuwa mchango huu utasaidia kuboresha sana hali ya ufaulu wa vijana wetu katika shule mbalimbali za msingi na sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili; shule maalum ambazo zilikuwa zinafaulisha sana zamani. Kwanza naendelea kuzipongeza shule hizo ikiwemo Tabora Boys ambayo imekuwa ikichangia sana kuinua ufaulu wa Mkoa wa Tabora na ni kweli kwamba baadi ya miundombinu yake iko katika hali ambayo inahitaji sana msaada na naomba niungane nae katika kuzifuatilia shule hizo ili tusaidiane katika kuzitendea haki.
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.
Kwa kuwa matatizo yanayowakabili wananchi wa Mkoa wa Tabora yanafanana kabisa na wananchi wa Mkoa wa Morogoro hususani katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki hasa katika shule ya Mkuyuni ambayo upungufu wa madarasa yanayohitajika ni zaidi ya 18, shule ya msingi Ngerengere Njia Nne madarasa 21 yanahitajika na shule ya msingi Mikese Fulwe madarasa zaidi ya 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kuwa uwezo wa halmashauri yetu ni mdogo na uwezo wa wananchi kujenga madarasa haya yote ni mdogo sana. Je, Serikali kuu ina mpango gani wa kutusaidia kumaliza tatizo hili la vyumba vya madarasa ili kuinua ubora katika shule zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba sana Mheshimwa Omari Tebweta Mgumba, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki nikutane naye baada tu ya Bunge mchana saa saba na nusu ili tuweze kupanga mikakati pamoja. (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Udhaifu katika sekta ya elimu ni mkubwa kwa nchi nzima na hiyo imekuwa ni mjadala kwa muda mrefu na Wabunge hapa wanaulizia miundombinu na mambo mengine kama walimu, mishahara, yapo ni mambo mtambuka. Sasa Serikali haioni umuhimu, ili elimu yetu iweze ikawa sawa, bora na shirikishi kwa wote, tukawa na mjadala wa Kitaifa namna ya kuboresha elimu kwa kuwa ndio tunda la mfumo wa maendeleo yote Tanzania?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimshukuru sanaMheshimiwa James Mbatia kwa kurejea kauli ambayo aliitoa Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, Rais wetu mstaafu kuhusu mjadala wa kitaifa ambao sasa hivi tunafikiria namna ya kuuandaa. Kwahiyo naomba ashiriki na sisi katika kuandaa mjadala huo.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri aliyonipa Mheshimiwa Waziri, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijauliza, nichukue fursa hii kuishukuru Serikali kwa sababu ya kazi kubwa na nzuri wanayoifanya kuinua hali ya elimu katika Wilaya ya Longido. Historia ya Wilaya ya Longido…
Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa. Swali ni kwamba kwa upande wa ubora wa elimu ukizingatia kwamba ubora wa elimu unategemea uboreshaji wa shule kuanzia ngazi ya chekechea; na kwa kwa sababu vitongoji vya Wilaya ya Longido viko mbali na shule za msingi zenye elimu za chekechea (shule za awali).
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ina mpango gani katika kuhimiza wananchi wajenge shule na Serikali ipeleke walimu waliosomea?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa kuwa tatizo la shule za msingi la miundombinu halina tofauti na Shule zetu za Sekondari katika Wilaya ya Longido; je, Serikali imejipangaje kutusaidia kuziba mapengo yaliyopo katika madarasa yapatayo 58, maabara 27, mabweni 73, nyumba za walimu
252, maktaba nane...
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna uhaba wa walimu wa sayansi wapatao 27? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS - TAWALAZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, katika muda mfupi tangu alipochaguliwa kuwa Mbunge amefanya mengi, ofisini kwangu ameshakuja zaidi ya mara tatu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi zake nazipokea kwa niaba ya Serikali, naomba sana nimhakikishie kwamba wananchi waendelee na juhudi wanazozifanya. Tunatambua juhudi zao. Pale ambapo atakamilisha darasa lolote la awali, tuwasiliane ili tuweze kupeleka walimu wa madarasa ya awali ambao wamesomeshwa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kuhusu kumalizia maboma ambayo wananchi wameanzisha na yamefika kwenye lenta, naomba nimhakikishie kwamba katika fedha za ruzuku ya maendeleo ambazo tutazipeleka kuanzia mwezi wa Saba tumewapa kipaumbele Wakurugenzi wazingatie sana kumalizia maboma ambayo yameanzishwa na wananchi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa ukosefu wa mabweni ni tatizo la nchi nzima na hasa katika shule za sekondari za kata, hivyo kufanya baadhi ya wanafunzi kupanga katika nyumba za watu binafsi; je, Serikali haioni umefikia wakati kuhamasisha wadau mbalimbali wa elimu kujenga hostel karibu na shule ili kuepuka kadhia hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalitambua sana tatizo la mabweni katika shule za sekondari za kata. Lengo la kujenga shule za sekondari za kata ilikuwa ni kuwawezesha watoto ambao wako ndani ya kata waweze kusoma, lakini tatizo ni kwamba kuna baadhi ya vijiji kweli viko mbali sana na Makao Makuu ya Kata au mbali sana na eneo ambalo ipo shule. Kwa hiyo, kuna tatizo kwamba wanafunzi wengi wamekuwa wakipanga nyumba kwa sababu hawawezi kutembea kilometa labda 15,20 kutoka nyumbani kwao kwenda katika shule kusoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo tatizo tunalielewa na ninaungana naye na tutaendelea kuhimiza wadau wajenge mabweni na hostel karibu na shule hizi ili kusudi ziweze kutoa huduma nzuri kwa watoto na hasa watoto wa kike waweze kuepuka matatizo mengine ambayo yanawapata kupanga katika nyumba za watu.
MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa kuuliza swali la nyongeza. Matatizo yaliyopo katika Jimbo la Longido ni sawa kabisa na matatizo ambayo yapo katika Jimbo la Ludewa. Jimbo la Ludewa kwa sasa lina upungufu wa walimu 500 wa shule za msingi. Je, Serikali ina mpango gani kutuletea walimu wa shule ya msingi katika Jimbo la Ludewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Deo Ngalawa kwa kunirejesha vizuri katika kumbukumbu zangu kwamba tunaendelea na mchakato chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi Baraza la Mitihani linaendelea kuchakata na kuvikagua vyeti vya walimu 1,0140 ambao tunategemea waajiriwe kwa ajili ya shule za msingi ifikapo tarehe 30 Juni, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Ngalawa tuendelee kuwasiliana ili tutakapofika wakati wa kuwapangia maeneo ya kwenda, basi tuwe na mawasiliano ya karibu. Ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Serikali ningependa niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; pamoja na maelezo haya bado Walimu hao wameendelea kuchangishwa michango na kwa sababu wanaowachangisha ni mabosi wao ikiwemo michango ya mwenge na Mwalimu asipokubali kuchanga michango anawajibishwa kule kwa sababu Waziri hayupo. Je, ni hatua gani zinachukuliwa kwa wakubwa wa Walimu hawa kwa maana ya Wakuu wa Idara za Elimu, Maafisa Elimu kama wataendelea kuwachangisha michango ya lazima kinyume na maelekezo ya Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kwa jibu hilo la Mheshimiwa Waziri ni wazi tunafahamu kwamba kuna waraka ulitembezwa ambao unatoa maelekezo, lakini baada ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais ilizuka sintofahamu na wananchi walikuwa wamechanga vyakula katika mashule mbalimbali wakaanza kugawana, kuna miradi ya kuchangia madawati, madarasa na kuta mbalimbali wakaanza kukataa. Je, ni hatua gani za dharura kwa Serikali ili kutoa maelekezo kwa wananchi na wadau mbalimbali wa elimu warudi kama zamani washirikiane Walimu na walezi wa shule hizi ili shughuli za maendeleo ziendelee kuwepo kwa maana ya kuondoa kero za elimu katika maeneo mbalimbali? (Makofi). Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, baadhi ya michango halali kwa mfano michango ya Mwenge inatakiwa ichangishwe kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya na sio vinginevyo. Hii michango haitakiwi kupitia kwenye Kamati za Shule wala mikutano ya wazazi katika shule, hiyo hairuhusiwi. Kwa hiyo, Kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya ndiyo inayoratibu masuala yote yanayohusu Mwenge michango ikiwepo michango ya mwenge.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili kuhusu sintofahamu ya michango iliyosababisha baadhi ya watu kwenda kudai michango ambayo walikuwa wamechanga hapo awali. Napenda nisisitize msimamo wa Serikali kwamba ilikuwa ni makosa hapo mwanzo tulivyokuwa tunachangisha kwa kuwahusisha Walimu kuwaondoa darasani wanafunzi kwa sababu tu wazazi wao labda kwa sababu ya umaskini wao hawakuwa wamechanga. Hilo lilikuwa ni kosa kwa sababu mtoto yule aliyekuwa anatolewa darasani hakuwa na kosa lolote.
Mheshimiwa Spika, maelekezo ya Mheshimiwa Rais yanasimama pale pale, isipokuwa utaratibu ambao sasa hivi tumeupitisha katika kutekeleza ule Waraka Na.5 wa Elimu kuhusu michango ni kwamba michango yote sasa itaratibiwa na Serikali za Vijiji na Kata chini ya usimamizi wa Mkurugenzi wa Halmashauri.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali ya Kijiji, Halmashauri ya Kijiji ikikutana ikapendekeza, wanapeleka kwenye Mkutano Mkuu wa Kijiji, wakikubaliana wanapeleka maamuzi yao kwenye Kamati ya Maendeleo ya Kata ambayo ikipitisha inapeleka kwa Mkurugenzi, Mkurugenzi anatoa idhini ya mchango ule kuchangwa. Mchango ukishachangwa ukikamilika taarifa inatolewa kwa Mkurugenzi ili hatua zaidi za utekelezaji ziendelee. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Hata hivyo, nitakuwa na maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wataalam wakati wa kuweka mipaka katika baadhi ya maeneo wamekuwa wakishirikisha upande mmoja badala ya kushirikisha pande zote mbili na hivyo kusababisha migogoro ya mipaka katika maeneo hayo hususani mipaka ya vijiji vyetu. Je, nini kauli ya Serikali ili kuondoka na tatizo hilo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kule Jimboni kwetu Mbinga Vijijini kuna migogoro ya mipaka kati ya Vijiji vya Kilagano, Lugagala na Liganga ambavyo vipo Jimbo la Peramiho, Songea Vijijini. Upande mwingine mgogoro huo unasisha Kijiji cha Litumbandyosi, Mabuni pamoja na Luhugara kwa upande wa Jimbo la Mbinga Vijijini. Je, lini Serikali itashuka ili kwenda kutatua mgogoro huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza kwamba wataalam wamekuwa hawashirikishi pande zote zinazohusika kwenye maeneo ya utawala, hilo ni tatizo na tumeshawapa maelekezo kwa sababu ya migogoro ambayo imesababishwa na kadhia hiyo. Hapa nchini tunayo jumla ya migogoro 366 ambayo imeibuliwa na Kamati ile ya Pamoja ya Wizara mbalimbali ambayo sasa hivi inashughulikiwa. Sasa hivi tumeshawaelekeza wataalam wetu wale wanaoratibu, wakienda kwenye eneo lolote watakapoanza upimaji upya lazima washirikishe pande zote mbili au pande zote zinazohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kuhusu migogoro inayoendelea chini ya uratibu wa Wizara ya Ardhi kitaifa, migogoro yote nchini imeanza kushughulikiwa tangu mwezi Aprili, 2018 na tunaimani mpaka mwisho wa mwaka huu migogoro yote itakuwa imeshughulikiwa ile ya kijiji kwa kijiji, kata kwa kata, wilaya kwa wilaya, mkoa kwa mkoa, maeneo ya wananchi na maliasili na maeneo mengine yote ambayo yana migogoro tuna imani kwamba mpaka mwisho mwa mwaka huu yatakuwa yametatuliwa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba kuuliza, hivi haionekani kwamba wanapokuja wataalam wa TAMISEMI kugawa upya vijiji na hata vitongoji wanaleta migogoro ambayo haiishi na maendeleo kusitishwa? Je, Waziri anasema nini kwa migogoro ambayo ipo na imewadhuru watu ambao wako kwenye maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye maswali ya nyongeza ya muuliza swali la msingi, migogoro yote inashughulikiwa isipokuwa kuna baadhi ya maeneo ambayo kulikuwa na matatizo ya usajili wa vijiji na vitongoji ambapo baada ya kupitia upya taratibu imeonekana kwamba kuna baadhi ya maeneo taratibu zilikiukwa.
Kwa hiyo, kule ambako taratibu zilikiukwa, pengine usajili wa kijiji au kitongoji ulipenyezwa bila kufuata utaratibu rasmi wa Serikali, maeneo hayo baadaye yamefanyiwa marejeo ya kufuta usajili wa kijiji au kitongoji. Kwa hiyo, suala hilo likishafanyika inakuwa siyo mgogoro tena. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kama kuna migogoro ya aina hiyo basi tuwasiliane ofisini kwa Katibu Mkuu wa TAMISEMI ili kuweza kufuatilia vizuri zaidi na kurekebisha.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa matatizo ya Mbinga Vijijini yanafanana kabisa na matatizo ya Jimbo la Mbagala katika Mkoa wa Dar es Salaam. Jimbo la Mbagala sasa hivi lina watu takribani watu 1,100,000. Idadi hii ya watu ni kubwa sana kiasi kwamba utoaji wa huduma katika jimbo hili unakuwa mgumu na miundombinu inaharibika mara kwa mara kutokana na wingi wa watu waliopo katika eneo hilo. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuligawanya Jimbo hili la Mbagala ili liweze kufikika na hata Mbunge aweze kutoa huduma zake kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza huyu ni ndugu yangu kabisa katika ukoo. Ni kweli Jimbo la Mbagala kwa idadi ya watu ni miongoni mwa majimbo yenye watu wengi ikiwemo Temeke na majimbo mengine hasa ya Dar es Salaam, lakini hivi karibu tumegawa majimbo ya Dar es Salaam. Kwa hiyo, nashauri kwa vigezo vile ambavyo nimevizungumza kwenye jibu la msingi, naomba sasa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke wakae ili waweze kupendekeza, lakini wapeleke mapendekezo yao moja kwa moja Tume ya Taifa ya Uchaguzi.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nami nina swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ugawaji wa maeneo ya utawala ngazi ya kata, tarafa na mitaa yaliyokosewa sana au kusahaulika katika Wilaya ya Kasulu. Unakuta kijiji kimoja chenye wakazi 10,000 ni mtaa mmoja, kijiji chenye wakazi 12,000 ni mtaa mmoja. Nina mifano halisi, kwa mfano wa Kijiji cha Nyantale ni kimoja na mtaa ni huo huo. Je, maeneo yaliyokosewa na kusahaulika ni lini sasa TAMISEMI wanakwenda kurekebisha kasoro hizo kwa sababu hazihitaji miundombinu wala uwekezaji wowote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba kuna baadhi ya maeneo wakati wa kutenga maeneo hayo yaliyokosewa, vigezo havikuangaliwa vizuri. Kwa sasa hivi kulingana na payroll iliyopo Serikalini ambayo bado tunaendelea kuirekebisha itakuwa vigumu sana ndani ya miaka hii miwili kumuahidi kwamba tutarekebisha mwaka ujao au mwaka 2020. Naomba sana wananchi katika maeneo hayo waweze kuwa na uvumilivu, kwa nchi nzima zoezi hilo litafanyika baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri ambayo yako sawasawa na matakwa ya Wanauyui, DCC pamoja na RCC. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa vile Serikali na wadau wengine wote wamekuwa wanalipa fedha zilizotakiwa kwenda Halmashauri ya Uyui, I mean Tabora District Council, zimekuwa zinalipwa halmashauri au manispaa; je, Serikali sasa itakuwa tayari kusaidia hela zote ambazo zimelipwa manispaa na manispaa wakazitumia, ili ziweze kurejeshwa katika Halmashauri ya Uyui?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa vile maelekezo ya Serikali ni kwamba, tukae sasa Baraza la Madiwani, DCC na RCC tuombe kubadilishiwa jina la Tabora Kaskazini ambalo halina Mashariki, Kusini wala Magharibi liweze kuwa Jimbo la Uyui. Je, Serikali, yeye Waziri ataunga mkono jambo hili ili liweze kupita haraka kama ambavyo tunapendekeza sisi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, kuhusu mkanganyiko wa jina, nataka nimwambie Mheshimiwa Maige na wadau wote wa Mkoa wa Tabora na nchi nzima kwamba hakuna mkanganyiko wowote wa jina; kwa sababu Halmashauri ya Manispaa ya Tabora hailingani kwa vyovyote vile na Halmashauri ya Wilaya ya Tabora, kwa hiyo, hakuna tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utendaji, wale watendaji wa Serikali wanaokosea kupeleka fedha za Halmashauri ya Wilaya ya Tabora wakazipeleka kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Tabora wamefanya makosa. Kwa hiyo, fedha zote ambazo zimekwenda Manispaa ya Tabora ambazo ni za Halmashauri ya Wilaya ya Tabora zinatakiwa zipelekwe Halmashauri ya Wilaya ya Tabora na kama kuna fedha zilikwenda kimakosa zirejeshwe haraka iwezekanavyo.
Mheshimiwa mwenyekit, katika swali lake la pili; sisi katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa sababu hatuna mamlaka na jina la jimbo, tunawaunga mkono Halmashauri ya Wilaya ya Tabora ambao pengine baada ya muda mfupi ujao itakuwa Halmashauri ya Wilaya ya Uyui. Wakipendekeza jina Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwamba, jina la Tabora Kaskazini sasa libadilishwe sisi tutawaunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwa kuwa, Halmashauri ya Geita iligawanywa mara mbili, Geita Mjini na Geita Vijijini; na kwamba mpaka sasa Ofisi za Mkurugenzi wa Geita Vijijini ziko mjini; je, TAMISEMI inafikiriaje kumhamisha Mkurugenzi wa Geita Vijijini kurudi vijijini ambako ni Nzela ili aweze kuwa karibu na wananchi wake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, swali hili la Mheshimiwa Musukuma ni swali la kiutendaji zaidi, naomba nilifanyie kazi baada ya kurudi ofisini.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Swali la kwanza; kwa kuwa, Serikali imekiri upungufu wa Walimu katika Wilaya ya Magu, je, itakapoajiri itanipangia Walimu wa kutosha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa bado tuna upungufu hasa wa Walimu wa sayansi. Serikali ina mkakati gani wa kuziba pengo hilo la Walimu wa sayansi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza kuhusu upungufu wa Walimu napenda nimhakikishie kwanza kwamba angalau Wilaya yake ya Magu ina nafuu kidogo. Kuna baadhi ya Halmashauri zina upungufu wa Walimu kwa chini ya asilimia 60 ya mahitaji. Angalau wilaya yake ina asilimia zaidi ya 70. Kwa hiyo tutakapoajiri tutapanga Walimu kulingana na uwiano wa upungufu uliopo nchi nzima. Kwa hiyo, asiwe na wasiwasi wowote.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili, kuhusu upungufu wa Walimu wa sayansi; tulikuwa na upungufu wa Walimu wa sayansi kama 19,000. Sasa tumejizatiti, tunaandaa utaratibu wa kuajiri Walimu wa sayansi kama Walimu 6,000 mpaka mwishoni mwa mwezi wa Sita. Tunaamini upungufu wa Walimu wa sayansi mpaka 2020/2021 hatutakuwa nao tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge zima kwamba tumejindaa vya kutosha kuhakikisha kwamba tunapunguza upungufu wa Walimu wote wa sayansi na wa shule za msingi.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, tatizo la upungufu wa Walimu katika Shule za Msingi Magu ni sawa kabisa na katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita. Je, Serikali inasemaje sasa kuweza kuhakikisha kwamba, suala hili linafanyiwa kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika majibu yaliyopita, ni kwamba chini ya usimamizi wa Mheshimiwa Rais wetu tunafanya jitihada za kutosha kuhakikisha kwamba tunapunguza kabisa tatizo la upungufu wa Walimu. Hatuwezi kulipunguza kwa siku moja au kwa mwaka mmoja kwa sababu mahitaji ni makubwa sana kulingana na payroll ya Serikali, lakini tunajitahidi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano tunataka tuondokane na upungufu wa Walimu wa sayansi, hadi mwaka 2020/2021 tuwe hatuna upungufu wa Walimu wa sayansi. Kwa upande wa shule za msingi tunataka tupambane kuhakikisha kwamba ndani ya miaka michache ijayo tumepunguza kabisa upungufu wa Walimu wa shule za msingi katika halmashauri zote, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Geita.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nataka kuwaambia tu Waheshimiwa Wabunge kuwa humu ndani kaingia mnyama mkali sana, lakini tuko salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali jana ilitoa kauli kuwa ili Tanzania ifanikiwe katika michezo ni lazima wachezaji wa timu ya youth watoke kwenye shule. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza Walimu kwenye shule, ili tuwe na oriented result youth team ya Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu, Mbunge wa Ilala na naungana naye kwenye furaha yake ambayo naijua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Zungu kwamba shule yetu au chuo chetu cha michezo pale Malya - Mwanza Serikali inakiboresha; na tutapeleka Walimu kwa awamu ili wakafundishwe, ukiacha wale ambao wanasoma kutoka mashuleni, tunataka tupeleke Walimu ambao watafundishwa masomo ya michezo kwa muda ili waje kuboresha michezo kwenye shule zao wanazofundisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tuna Walimu ambao wana uzoefu wa michezo, wengi tu ambao wanafundisha na Walimu wa michezo wako wachache. Nataka nitoe rai kwa Maafisa Elimu wote nchi nzima, kwamba Walimu wetu ambao wanafundisha michezo, wale ambao hawana cheti cha michezo basi wawape kipaumbele kuwapeleka kwenye chuo chetu cha michezo ili hatimaye tupate timu nzuri kwanza ya UMITASHUMTA na timu nzuri ya UMISETA ambayo itakuwa inapambana vizuri na nchi nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo tumeona mwaka huu zimepambana timu zetu za vijana na kushinda huko nje, inawezekana kabisa tukapata Timu ya Taifa bora kabisa kutoka kwenye shule zetu na vyuo vyetu baada ya muda mfupi ujao.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo TAMISEMI na Waziri anafahamu, Halmashauri ya Lushoto ina upungufu wa Walimu 826 wa shule za msingi. Sasa Serikali inatuambia nini kuhusu huu usumbufu ambao umesababishwa na Wizara yenyewe? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid Shangazi, ambaye juzi alikuwa Singida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nikanushe kwamba upungufu wa Walimu haujasababishwa na Wizara yetu kwa sababu upungufu wa watumishi uko kwenye kila sekta na si sekta ya elimu peke yake. Tunafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha kwamba tunapunguza upungufu wa watumishi kwa Serikali nzima kwa sekta zote. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Shangazi kwamba tutakapokuwa tunaajiri na tutakapokuwa tunahamisha Walimu Halmashauri yake na Jimbo lake la Lushoto hatutaliacha nyuma.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa katika kuziimarisha tawala za mikoa ni pamoja na kuziruhusu na kuzipa uwezo wa kufanya maamuzi yake zenyewe, ikiwemo kuwapangia vituo watumishi wapya ambao wanaajiriwa. Hata hivyo, lakini hivi karibuni Serikali mmebadilisha utaratibu, wanaoajiriwa hasa walimu mnawapangia vituo kutoka makao makuu, wenyewe, badala ya kupangiwa kule kwenye halmashauri ambako ndiko wanakojua mahitaji ya Walimu katika maeneo yao. Kwa nini Serikali wamepora madaraka ya Tawala za Mikoa, hasa Halmashauri, kupanga vituo vya watumishi? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uliokuwa unatumika zamani ulikuwa ni kwamba Serikali ikishaajiri basi lile rundo la waajiriwa au idadi ya waajiriwa inapelekwa katika halmashauri. Hapo inakuwa ni kazi ya halmashauri kuwapangia mahali pa kwenda kufanya kazi au vituo vya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyopatikana kutokana na utaratibu huo ambao wenzetu walipata shida sana kuudhibiti ni vi-memo, vikiwemo vi-memo vya Wabunge. Akishapelekwa katika halmashauri fulani ki-memo kinafuata bwana huyo ni wa kwangu kwa hiyo msimpangie mbali na mji. Kwa hiyo unakuta Walimu wengi walipangiwa katika maeneo ya Makao Makuu ya Wilaya, katika maeneo ya miji hasa wanawake, sitaki kueleza sababu kwa sababu gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Nnauye kwamba baada ya kupata changamoto hiyo sasa Serikali imeamua kwamba tunapowapeleka; kwa sababu Maafisa Elimu wanakuwa wameleta yale mahitaji ya kila shule katika halmashauri yake; tunajua kwamba Yaleyale Puna wana Walimu saba, tunajua kwamba Pemba Mnazi wana Walimu watatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunajua kwamba kutoka makao makuu tupeleke Walimu watano Pemba Mnazi na tupeleke Walimu wawili Yaleyale Puna ili kusudi shule za pembezoni nazo zipate Walimu badala ya kupeleka vi-memo kwa Afisa Elimu. Ki-memo cha Mbunge kina nguvu sana kwa Afisa Elimu lakini ukileta ki–memo kwangu kinadunda tu, wala hakiwezi kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Nape Nnauye wala asipate wasiwasi, tunafanya hivyo kwa ajili ya kuangalia kwamba kunakuwa na usawa mkubwa kwa wale ambao wana uhitaji mkubwa wa kupewa Walimu. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Sekta za Elimu na Afya ni sekta ambazo zinaongoza kwa upungufu wa watumishi hapa nchini na tunaelewa Sekta ya Elimu inaandaa rasilimali watu wa Taifa na Sekta ya Afya inaenda kuhudumia hii rasilimali watu ili Taifa liweze kusonga mbele. Hata hivyo, upungufu umekuwa mkubwa sana kwenye hizi sekta mbili hasa. Nini mkakati wa Serikali wa muda mfupi na wa muda mrefu wa kuhakikisha kwamba sekta hizi angalau kwa asilimia 60 mpaka 70 zinapata watumishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, nadhani nimepatia sasa maana huwa ninakosea kosea sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii najibu kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na kwa niaba ya Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, ambaye ni baba yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hadi sasa imetoa kibali cha kuajiri watumishi 52,000. Katika hao watumishi 52,000 kipaumbele kikubwa kimeelekezwa kwenye sekta hizi mbili, Sekta ya Elimu na Sekta ya Afya ambazo kwa pamoja zitakuwa na waajiriwa wapya wapatao 33,000 ambao ni zaidi ya asilimia 50 ya waajiriwa wote ambao wataajiriwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Paresso na Waheshimiwa Wabunge wote wa-support huu mchakato unaoendelea ambao utapunguza sana mahitaji au upungufu wa watumishi katika sekta hizi mbili ambazo ni muhimu sana katika nchi yetu. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze vijana wetu wa Timu ya Simba, wamefanya kazi nzuri sana ya kutwaa ubingwa kabla ya mechi zingine hawajacheza, hongereni sana. (Makofi/ vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili; mwaka 2011 aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Mizengo Pinda alitangaza kwamba Mima sasa ni Tarafa itakayokuwa na Kata za Berege, Kitemo, Mima, Ihondwe na Mkanana. Sasa ni miaka 11 hakuna hata jengo; na hizo Sh.50,000,000 sijaziona. Sasa nataka nimuulize swali Mheshimiwa Naibu Waziri, haya yalikuwa ni matamshi ya mdomo tu au hiyo tarafa ipo kwenye Gazeti la Serikali?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Tarafa hii ya Mima ina miundombinu mibovu sana; barabara zote hazipitiki, kuanzia Gulwe kuja Berege, Chitemo, hapa Mima Sazima, Igweji Moja, Igweji Mbili mpaka Seruka na kutoka Igweji moja kwenda Ihondwe njia ya mkato hazipitiki. Je, Mheshimiwa Waziri ana maelezo gani kwa wananchi wa Jimbo la Mpwapwa na hasa Tarafa ya Mima?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia angalia labda kuna Waziri amesimama lakini basi nitaendelea kulijibu mimi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Lubeleje ni maswali magumu, na mimi napenda kuyajibu kama ifuatavyo. Ni kweli kwamba Mheshimiwa Mizengo Pinda alitangaza Tarafa ya Mima kuwa Tarafa mwaka 2011, wakati huo alikuwa Waziri Mkuu lakini ndiye alikuwa Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie kwamba Tarafa ya Mima sawasawa na Tarafa nyingine imetangazwa kwenye Gazeti la Serikali na ndiyo maana akateuliwa Afisa Tarafa Maalum kwa ajili ya tarafa hiyo, kwa hiyo tunaitambua. Hizi Sh.50,000,000 amesema hajaziona, ni kweli hajaziona kwa sababu bado hazijapelekwa. Tunajiandaa kuzipeleka hivi karibuni na tumemwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri kwamba atakapopata hizi fedha azi-commit haraka kwenye kazi ili kusudi kazi iweze kufanyika ya kujenga Ofisi ya Afisa Tarafa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, kuhusu miundombinu; nchi yetu imekumbwa na matatizo makubwa sana hivi karibuni baada ya mvua kubwa kunyesha, maeneo mengi sana miundombinu imeharibika. Kwa hiyo hili najua ni swali la Wabunge wengi, lakini kwa Mima anaulizia kwa sababu kwa kweli kuna barabara huko hazijawahi kutobolewa na mambo mengine mengi na kazi ya kutoboa barabara ni kazi ya halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana nikitoka hapa Bungeni niweze kumtuma Mkurugenzi wetu wa Miundombinu atembelee Tarafa ya Mima. Baada ya hapo tutapata majibu mazuri zaidi.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Serikali imeziagiza halmashauri ziwasilishe miradi viporo ambayo ilihubiriwa na wananchi isiyozidi kiasi cha shilingi bilioni 1 na kwamba fedha hizo zitaletwa katika mwaka huu wa fedha ili kuwapa wananchi nguvu waweze kumalizia miradi ile ambayo waliianzisha kwa nguvu zao. Je, ni lini Serikali sasa inaleta fedha zile kwa sababu umebaki takriban mwezi mmoja mwaka wa fedha kuisha na ni Serikali yenyewe ndiyo ilituambia sisi halmashauri tulete hizo fedha?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, pale Mafinga tunakusudia kukamilisha Kituo cha Afya cha Bumilayinga pamoja na zahanati mbili na kujenga nyumba za watumishi kwa maana ya wauguzi watakaoishi katika hizo nyumba kwenye Kituo cha Afya cha Bumilayinga na zahanati mbili za Ulole na Kisada pamoja na ile zahanati ya Sao-Hill. Je, ni lini Serikali inatuletea fedha ili tukamilishe miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tulielekeza orodha ya miradi viporo iletwe TAMISEMI lakini hiyo ilikuwa ni kwa ajili ya kujipanga vizuri kuweza kuwasaidia au kuunga mkono nguvu za wananchi. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Chumi na Waheshimiwa Wabunge wote kwenye halmashauri zao wawe na subira wakati Serikali inaendelea kujipanga. (Makofi)
MHE. DKT. TULIA ACKSON: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo hili la Rungwe ni kubwa sana. Hiyo ahadi iliyotolewa hapo na Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusu Kituo cha Mpuguso na Isongole, ndiyo, wadau wameendelea kuchangia lakini sijasikia namna ambavyo Serikali imejipanga. Kwa sababu amesema shilingi milioni 100 zitatoka katika mapato ya ndani, hayo yamekuwepo kila wakati, je, Serikali imejipangaje? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Mbunge wa Kuteuliwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika jibu la msingi nimeeleza kwamba halmashauri ya wilaya imetenga shilingi milioni 100 kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa OPD katika Kituo cha Afya cha Mpuguso ambacho wameanza wenyewe kujenga kwa kushirikiana na wananchi. Nimetoa ahadi kwamba Serikali katika mwaka 2018/2019 itahakikisha kwamba vituo hivi viwili; cha Mpuguso na Isongole vinakamilishwa kwa utaratibu uleule ambao tumeutekeleza mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, kwa Rungwe, tutakuwa na vituo hivyo viwili kwa kuanzia. Naomba sana Mheshimiwa Mbunge tuwe na mawasiliano ya karibu, inapofika mwezi wa Agosti au Septemba kusudi tuhakikishe kwamba vituo hivi viwili vinapatiwa fedha za ujenzi ili viweze kukamilika 2018/ 2019.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapo hapo tuendelee kuwa na mawasiliano ya karibu kwa sababu Jimbo la Rungwe ni kubwa sana ili kusudi tuangalie na maeneo mengine.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika kuipunguzia mzigo Hospitali ya Halmashauri ya Mji, Kondoa ambayo inahudumia zaidi ya halmashauri tatu, zahanati za Kata mbili za Kolo pamoja na Kingale zimewekwa katika mpango wa kupandishwa hadhi na kuwa vituo vya afya. Je, ni lini sasa Serikali italeta hizo fedha kwa ajili ya kutekeleza hiyo awamu ya kuweka vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (ME. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Edwin Sannda, Mbunge Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Zahanati za Kolo na Kingale zikipandishwa hadhi zinaweza sana kupunguzia mzigo hospitali ya wilaya. Kama nilivyojibu swali la Mheshimiwa Dkt. Tulia, naomba awe karibu sana kimawasiliano, mwezi Agosti na Septemba ili tuone namna ya kuzipatia fedha zahanati hizi hatimaye ziweze kupandishwa hadhi na Wizara ya Afya ziwe vituo vya afya.
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na majibu ya Serikali ni dhahiri kwamba mafunzo haya hayafuatiliwi ndiyo maana sasa wanaagiza. Katika mafunzo yanayotolewa hayahusu mafunzo ya ukakamavu, je, Serikali iko tayari kuweka mpango wa kuwapeleka baadhi ya Watendaji wa vijiji kupata mafunzo ya JKT ili kusudi kuwaimarisha kiutumishi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika kutekeleza majukumu yao, Watendaji wa Vijiji wamekuwa wakipata madhara ikiwemo kudondoka na pikipiki na wengine kuumizwa na wananchi. Ni nani anayewajibika kuwalipa fidia pale wanapokuwa wamepata madhara hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwalongo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, napenda kumpongeza sana kwa sababu anahitaji sana Watendaji wetu wawe wakakamavu. Napenda kumpa taarifa na kulipa taarifa Bunge lako Tukufu kwamba wale Watendaji wote ambao walipitia JKT kwa mujibu wa sheria kabla utaratibu huo haujasimamishwa kwa muda, hao hawahitaji kupatiwa mafunzo tena kwa sababu tayari hao ni service girls and women. Kwa hiyo, wale ambao hawakupitia mafunzo hayo, tumepokea wazo lake zuri, tutaandaa utaratibu siyo lazima kuwapeleka JKT bali wanaweza wakahudhuria mafunzo ya mgambo ambayo huendeshwa na Washauri wa Mgambo katika wilaya zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili kuhusu fidia, zipo Sheria za Utumishi zinazoelekeza kuhusu fidia. Kwa hiyo, suala hili kwa sababu ni la kisheria, naomba sana watumishi wote ambao wanapata ajali au kuumia kazini sheria zipo zitumike. Ahsante sana.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunikumbuka maana mara nyingi sikumbukwi kwenye maswali ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu liko sawasawa na la Mheshimiwa Mwalongo, ni kwamba kwenye Jimbo langu la Same Mashariki unakuta kata na vijiji hazina Watendaji, badala yake wanatumiwa Maafisa Ugani na wala wao hawana mafunzo ya kufanya kazi za utendaji. Ni lini Jimbo la Same Mashariki litasaidiwa ili tupate watendaji ambao wanakidhi hadhi ya kazi hiyo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Naghenjwa Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba katika nchi tuna tatizo kubwa la Watendaji hasa ngazi ya Watendaji wa Kata na Vijiji. Maeneo/halmashauri nyingi zina upungufu mkubwa sana wa Watendaji wa Kata na Watendaji wa Vijiji. Kwa hiyo, kutokana na upungufu huo wamekuwa wakitumika maafisa, wakati mwingine Maafisa Elimu wa Kata, Maafisa Ugani, Maafisa Kilimo wanakaimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa suala hili kwa sababu tunaliweka katika utaratibu wa kuomba vibali vya utumishi, napenda kuahidi nchi nzima kwamba suala hili litakuwa limekwisha ifikapo mwaka 2020.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa pamoja na mafunzo ambayo wanapata Watendaji wa Vijiji katika utekelezaji wanakwenda kushirikiana na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, Vitongoji na Vijiji ambao wamekuwa wakilalamikia sana kuhusu maslahi yao. Napenda kujua, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha maslahi ya Wenyeviti wa Serikali za Vijiji na Vitongoji pamoja na kupewa mafunzo kama watakayopewa Watendaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema kwamba tunafanya mafunzo mengi kwa ajili ya Watendaji, lakini napenda nimhakikishie kwamba mafunzo ya aina nyingi vilevile, hasa ya uongozi yamekuwa yakitolea kwa Wenyeviti wa Serikali za Vitongoji, Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Madiwani na viongozi wengine wa kuchaguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu maslahi, suala hilo kwa sababu liko katika maelekezo ya Serikali kwamba walipwe kupitia 20% zile za mapato ya ndani ya halmashauri, napenda kumuahidi kwamba mimi mwenyewe nitaanza ufuatiliaji wa karibu sana kuanzia mwaka ujao wa fedha ili kuhakikisha kwamba Wenyeviti wa Vitongoji na Vijiji wanalipwa.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa Wabunge wa Viti Maalum ni Wabunge sawa na Wabunge wa Majimbo, hivyo basi, Serikali haioni kwamba kuwanyima Wabunge wa Viti Maalum kuhudhuria kwenye Kamati za Fedha inawasababisha wasielewe mipango ya fedha kwenye Halmashauri zao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kwa nini basi hii sheria isiletwe humu Bungeni ikabadilishwa ili kuweka usawa na kuondoa ubaguzi wa jinsia kwa sababu kutomruhusu Mbunge wa Viti Maalum kuingia kwenye Kamati za Fedha ni ubaguzi wa jinsia ya mwanamke na mwanaume ambayo inaanzia kwenye sheria zetu za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, ni kweli kama alivyosema ni vigumu sana kujua kwa kina yale ambayo yamejadiliwa na kikao husika kama wewe siyo Mjumbe. Hiyo ni kweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kuhusu kwa nini Serikali isilete Bungeni marekebisho ya sheria ili kusudi Wabunge wa Viti Maalum wawe Wajumbe, naomba tu nilipokee hili sasa kwa niaba ya Serikali ili tukalizungumze ndani ya Serikali kwa kuwa Vyama vya Siasa ambavyo viliwateua Wabunge wa Viti Maalum na kila Mbunge wa Viti Maalum amepangiwa Halmashauri fulani ya kuhudhuria vikao na kupiga kura. Basi nadhani hiyo inaweza ikawa ni mwanzo mzuri wa kuangalia ni namna gani tuweze kuleta marekebisho ya hiyo sheria. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Wabunge wa Viti Maalum wamekuwa na majukumu makubwa sana ndani ya mikoa yao; je, ni lini sasa Serikali itaanza kuwapatia Wabunge wa Viti Maalum Mifuko ya Jimbo kama walivyo Wabunge wa Majimbo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli mapendekezo yamekuwepo mengi nje na ndani ya Bunge kuhusu Wabunge wa Viti Maalum nao kupewa sehemu ya fedha kama Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa maelekezo yaliyoko kwenye sheria hiyo, mpaka sasa hivi bado Wabunge wa Viti Maalum hawajaingizwa kwenye huo mfumo. Sasa kwa sababu ni pendekezo ambalo linahitaji majadiliano ya awali ndani ya Serikali kwanza, naomba nalo nilichukue.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Wabunge wa Viti Maalum uwakilishi wao uko kimkoa, lakini sasa Wabunge hawa wa Viti Maalum wamekuwa wakipata changamoto nyingi katika kutekeleza majukumu yao ya Kibunge hususan katika kufanya mikutano ya hadhara. Sasa ni nini kauli ya Serikali katika hili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la mikutano ya hadhara linahusisha idara nyingi, ikiwemo Idara ya Polisi ambayo iko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu kwamba kama kuna mawasiliano mazuri kati ya Wabunge wa Viti Maalum na mamlaka zinazohusika, wakiwemo Wabunge wa Majimbo, hakuna matatizo yoyote. Inawezekana ukaandaliwa mkutano, hasa Mbunge wa Jimbo anaweza akaandaa mkutano ambao vilevile utahutubiwa na Mbunge wa Viti Maalum kwenye eneo lake. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa asilimia 10 inayotengwa kwa ajili ya wanawake, vijana na walemavu katika Halmashauri mbalimbali katika nchi yetu zimekuwa ni jambo ambalo halijatungiwa sheria, kwa hiyo, linatoa loophole kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zetu ama kupeleka au kutopeleka.
Je, ni lini Serikali itatunga sheria au italeta marekebisho ya sheria hapa Bungeni ili jambo hili la asilimia 10 kwa makundi haya iwe ni lazima na isiwe kama vile ambavyo wanafanya Wakurugenzi kwenye maeneo mbalimbali kwamba wanafanya kwa hiari? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira kidogo kwa sababu mwezi wa sita wakati wa kupitisha Sheria ya Fedha ya mwaka 2018 kutakuwa na kipengele ambacho kitamruhusu Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kutunga Kanuni ambazo zitawalazimisha Wakurugenzi kuhakikisha kwamba wanatenga fedha hizo asilimia 10 kama alivyopendekeza.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Hii asilimia 10 ambayo tunaizungumza ni ile inayotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri. Sote tutakuwa mashahidi kwamba ziko Halmashauri hazina uwezo wa kukusanya vyanzo vya mapato, wana vyanzo vidogo na vile vyanzo vingine vimechukuliwa na Serikali Kuu. Hii inasababisha kushindwa kutenga hii asilimia 10 kwa ajili ya wanawake, vijana na walemavu. Ni nini kauli ya Serikali katika kuhakikisha tunazipa uwezo Halmashauri ili ziweze kutenga hizi pesa kwa ajili ya kukopesha wanawake, vijana na walemavu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tumetoa maelekezo kwamba Halmashauri zote zifanye mapitio ya vyanzo vyao vya mapato ili kuhakikisha kwamba wanaongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato ya ndani na pili ni kwamba hata kama wamekusanya shilingi 10; asilimia 10 iko pale pale. Asitoe vigezo kwamba eti kwa sababu amekusanya mapato kidogo, basi atenge hiyo asilimia 10. Asilimia 10 ni ya kisheria na kwa mujibu wa maelekezo. Kwa hiyo, hata kama amekusanya 100 asilimia 10 iko pale pale.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa kuimarisha Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC), kutokana na changamoto nyingi zinazowakabili walimu na matatizo mengi.
Swali la kwanza, ni kwamba, je, Serikali iko tayari kuwatuma wataalam kwa mfano Kenya kwenda kujifunza jinsi ambavyo wenzetu wameweza kuimarisha chombo kama hiki cha TSC ili kifanikishe katika utoaji wa huduma kwa walimu kwa kuwa nao Kenya walikuja kujifunza kutoka kwetu, wao wakaenda wakaimarisha wakafanikisha?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali iko tayari baada ya kuwatuma wataalam Kenya kujifunza jinsi ambavyo wamefanikisha wenzetu, kurudi huku na wahakikishe kwamba, wanachukua hatua za kuimarisha, ili kifanikishe katika kutoa huduma kwa walimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nieleze kidogo kuhusu Mheshimiwa Mama Margaret Sitta. Mheshimiwa Sitta ni hazina kubwa ya kumbukumbu na uzoefu katika sekta ya elimu nchini kama Mwalimu, Afisa Elimu, Kiongozi wa Chama cha Walimu, Waziri na Mbunge. Kwa hiyo, kwa kweli, amekuwa msaada mkubwa sana kwetu Serikali katika kutoa mawazo ya kuiboresha zaidi sekta ya elimu na sisi tutaendelea kufaidika nayo.
Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo, kwa pamoja:-
Mheshimiwa Spika, kwamba ushauri wake wa kwenda kujifunza katika nchi ya Kenya tumeupokea na tutaufanyia kazi. Mapendekezo na ushauri wake katika suala la pili nao tunaupokea na tutaufanyia kazi, ili kuboresha zaidi Tume ya Utumishi wa Walimu. (Makofi)
MHE. NASSOR SULEIMAN OMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Serikali ilitoa kauli kwa wale wote walioathirika na zoezi hili kimakosa; Je Serikali imeshawarejesha?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuna wale ambao walioathirika kimakosa na wako karibu na kustaafu; je Serikali ina kauli gani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba baada ya zoezi hili yalitokea manung’uniko na vilevile zilitokea rufaa mbalimbali za watumishi ambao walidhani kwamba wameonewa. Serikali ilifanya uchambuzi wa kina, wale ambao walionekana kwamba kulikuwa na makosa katika mchakato huo wamesharejeshwa kazini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ameuliza swali lingine kwamba wale ambao walikuwa wanakaribia kustaafu Serikali imewaangalia namna gani? Ukweli ni kwamba kwa makosa ambayo walikuwa wameyafanya walitakiwa wapelekwe Mahakamani, lakini Serikali ilisema tuwasamehe mambo ya kuwapeleka mahakamani kwa makosa ya kughushi na wao wasilete madai mengine.

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kwanza kupongeza majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini napenda tu kuongezea kuhusiana na idadi ya waliokata rufaa na kurudishwa kazini, jumla ni watumishi 1,907. Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.(Makofi)
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mheshimiwa Naibu Waziri katika jibu la msingi amesema kwamba jumla ya Walimu 3,655 walipoteza kazi baada ya uhakiki na kugundulika na vyeti feki. Nataka kujua tu katika mwaka 2016/2017 na 2017/2018 Serikali kama ilipoteza Walimu hawa; je, hadi sasa imeajiri Walimu wangapi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya zoezi hilo kukamilika Serikali katika miaka hii miwili 2016/2017 na 2017/2018 imeajiri jumla ya Walimu 6,495. Kati ya hao Walimu wa shule za sekondari wa masomo ya sayansi na hisabati ni 3,728 na Walimu wa shule za msingi ni 2,767. Idadi hiyo ni zaidi ya walioachishwa kazi ni kwa sababu ya kuwa na vyeti vya kughushi.
MHE. OMARI A. KIGODA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya halmashauri bado zinalalamikiwa kwamba utekelezaji huu ni mdogo au wakati mwingine haufanyiki kabisa. Je, malalamiko haya yanapotokea katika baadhi ya halmashauri, hawa vijana, walemavu na akina mama, ni wapi wanapaswa waende kulalamika ili kuhakikisha utaratibu huu unafanyika? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Omari Abdallah Kigoda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama alivyosema hapo awali, ni kweli kwamba hatua ya kwanza kabisa ya kusemewa ni kwa Mheshimiwa Diwani, lakini vilevile kupitia Baraza la Madiwani ambacho ndicho kikao cha kwanza kabisa kuhoji kuhusu mgawanyo wa fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya mikopo ya vijana na wanawake.
Mheshimiwa Spika, lakini katika ukaguzi ambao wamekuwa wakiufanya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali amekuwa akionesha kwamba halmashauri ambazo hazitengi fedha kikamilifu kama ambavyo mapato ya ndani yanaonesha zimekuwa zinaandikiwa madeni. Kwa hiyo, uwajibikaji unaanzia hapo na hatua hizi tutaendelea kuzifuatilia. Kama nilivyosema katika jibu la msingi kwamba tunatarajia kuweka kipengele kwenye sheria ambacho kitalazimisha sasa kila halmashauri itenge asilimia 10 ya mapato yake ya ndani na itoe fedha hizo kwa ajili ya vikundi vya vijana na wanawake. (Makofi)
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hii asilimia 10 ya vijana na akina mama hii ni revolving fund, mtu anakopa, anarejesha. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, hawa tunaowakopesha, je, wanarejesha na kama hawarejeshi, wanachukuliwa hatua gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lubeleje, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba fedha hizi wanapokopeshwa vikundi vya vijana na wanawake wanatakiwa kurejesha na mratibu mkuu wa marejesho ni Afisa Maendeleo ya Jamii katika halmashauri husika. Kwa hiyo, kama kuna sehemu hawarejeshi kabisa, huo utakuwa ni udhaifu mkubwa sana wa kikazi wa huyo Afisa Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati yake ya Mikopo ya Halmashauri. Wito ambao tunautoa ni kwamba ni lazima wanaokopeshwa warejeshe, vinginevyo hatua zitachukuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo zuri kabisa ambalo amelifanya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI wakati anawasilisha hotuba ya bajeti ni kutoa tangazo kwamba kuanzia mwakani atafuta au amefuta riba kwenye mikopo ya wanawake na vijana. Kwa hiyo, hiyo iwe kichocheo cha mwananchi yeyote atakayekopeshwa mikopo hiyo arudishe fedha kama alizokopa bila riba. (Makofi)
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nishukuru kwa majibu hayo ambayo yamejibiwa sasa hivi lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Madiwani wanafanya kazi sawa na Wabunge. Kwa nini Serikali isiwalipe mishahara kama ambavyo Wabunge wanapewa mishahara? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kwa nini Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, sasa hivi Serikali haijaona umuhimu wa kuwalipa posho ambayo wanastahili kupata maana wanalipwa posho ndogo sana. Serikali ingeona umuhimu kwa sababu wao wanasimamia kazi za miradi ya maendeleo katika mitaa. Kwa hiyo, ningeomba sasa Serikali ifanye maamuzi ya kuwaongezea posho ili waweze kukidhi mahitaji yao. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) : Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza, ni kweli kwamba Madiwani wamekuwa na mtazamo huo wa kuomba kwamba kuwe na malipo hayo ya mshahara, Serikali iliyapokea na hata wakati Rais alivyohudhuria kikao cha ALAT mwaka jana alipokea maombi yao. Mimi nasema tu kwamba majibu yaliyotolewa pale ndiyo sahihi na hadi hapo Serikali itakapotoa maelekezo mengine lakini kwa sasa hivi tutaendelea na utaratibu ambao tunao.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili kuhusu Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Vitongoji na Mitaa kwamba posho ni ndogo sana, msisitizo ambao tunautoa sisi kila Halmashauri ifanye mapitio (review) ya vyanzo vyake vya ndani pamoja na mbinu zao za makusanyo, wakusanye kiwango cha kutosha cha mapato ya ndani na wahakikishe kwanza, hata hiyo ndogo maana maeneo mengine mengi tuna malalamiko kwamba hawalipi, hata hiyo ndogo basi inalipwa baada ya hapo sasa ndiyo tutaona tunaendaje huko mbele. (Makofi)
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Posho ya Wenyeviti wa Serikali za Vijiji kwenye Halmashauri zingine hawalipwi kabisa. Sasa nataka niulize tu swali kwa nini Wizara ya TAMISEMI isitoe Waraka Maalum kwenda chini kwa Wakurugenzi wote kuwaelekeza kwamba katika own source za Halmashauri wawe wanatoa kiasi fulani kwa ajili ya Wenyeviti wa Vijiji huku tukijua hao ndiyo wanaotusaidia kufanya kazi kubwa za maendeleo kwa niaba ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) : Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika swali la msingi, huo Waraka ambao Mheshimiwa Mbunge anaupendekeza ulitolewa mwaka 2003, lakini kwa sababu umekuwa ni wa muda mrefu pengine labda baadhi ya wenzetu wanaanza kuusahau, basi tutachukua ushauri wake ili tutoe maelekezo tena.
Mheshimiwa Spika, msisitizo ni kwamba lazima Halmashauri zote zifanye mapitio ya vyanzo vyao vya mapato, waongeze mbinu za ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kusudi wawe na uwezo mzuri wa kuweza kulipa. Hii ni kwa sababu hata taarifa za CAG zinaonesha kwamba ile asilimia 20 katika baadhi ya Halmashauri imekuwa hairudi kule kwenye vijiji kwa sababu tu ya malalamiko kwamba wamekusanya kidogo sana. Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mimi ni Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Mstaafu, Mtaa wa Kivule. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kitendo cha Serikali kutokutoa maelekezo mahsusi ya Wenyeviti wa Mitaa kulipwa posho inapelekea mzigo huu kupelekwa kwa wananchi ndiyo matokeo ya zile barua ambazo zinalipiwa, wananchi wanatwishwa mzigo huu. Kwa hiyo, ningeomba nijue, kwa kuwa Serikali imechukua vyanzo mbalimbali vya mapato kutoka Halmashauri na Halmashauri haipeleki fedha hizo kulipa Wenyeviti wa Mitaa na wanafanya kazi kubwa masaa 24.
Mheshimiwa Spika, ni kwa nini isiwekwe sheria moja kwa moja ili wadai kama haki? Kwa sababu sasa hivi ni posho kwa hiyo hawana uhalali wowote ule, Halmashauri inaamua ilipe ama asilipe. Ni kwa nini Serikali isiwajali watu ambao ni wengi sana katika nchi hii, wanafanya kazi kubwa sana ya miradi, ulinzi na usalama, usafi na ku-impose sheria mbalimbali walipwe pesa ya kisheria badala ya hii ambayo ni hiari? Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) : Mheshimiwa Spika, kama anavyosema ni kweli Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Vitongoji na Mitaa wanafanya kazi kubwa na nyingi na kweli mzigo ni mkubwa sana kwa upande wao. Sisi kama Wabunge na Serikali tunawategemea sana katika kazi zetu za kila siku. Ili kazi zetu na za Serikali ziende lazima wale wafanye kazi.
Mheshimiwa Spika, sasa mapendekezo ambayo anayatoa na kuhusisha kwamba Serikali imechukua vyanzo vingi vya mapato kwenye Halmashauri, mimi nataka nimhakikishie kwanza kwamba vyanzo ambavyo vimechukuliwa siyo vingi…
Mheshimiwa Spika, vyanzo vingi bado vipo katika Halmashauri na ndiyo maana tumewaambia kwamba wafanye mapitio. Wakishafanya mapitio Halmashauri ambayo itakuwa na changamoto za ziada basi wataleta taarifa TAMISEMI na tutaweza kuifanyia kazi.
MHE. SONIA J. MAGOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha na kujenga nyumba za walimu ili kuondoa adha ya tatizo hili ambalo limekuwa kubwa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha miundombinu ya majengo ya shule nyingi ambazo kipindi cha mvua watoto wamekuwa wakipata wakati mgumu? (Makofi) Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sonia Jumaa Magogo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kama tulivyojibu kwenye jibu la swali la msingi ni kwamba tunayo changamoto kubwa sana katika nchi ambayo ilitokana na kutekeleza mpango wetu wa maendeleo wa elimu ambao sasa hivi kuanzia mwaka 2015 mwezi Desemba, tunatoa Elimu Msingi Bila Malipo. Hiyo imevutia wanafunzi wengi zaidi kudahiliwa katika shule kuanzia elimu ya awali, elimu ya msingi na sekondari. Kwa hiyo, tuna uhaba mkubwa sana wa madarasa, nyumba za walimu na vyoo.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa Serikali imejenga vyumba vya madarasa, nyumba za walimu, matundu ya vyoo katika shule za msingi 6,200 nchi nzima na kazi bado inaendelea, tunaendelea kufanya hivyo kwa kushirikiana na wananchi. Katika shule za sekondari tumezifikia shule za sekondari 3,159, hii ni kazi kubwa na ndiyo maana nikatoa wito kwamba jambo hili haliwezi kufanywa na Serikali peke yake, tuna jumla ya shule 22,000 za msingi na sekondari. Sasa kama tumefikia shule 9,000 bado tuna kazi kubwa ya kufanya, tunataka mpaka ifikapo mwaka 2020 angalau tuwe tumezifikia shule 17,000, hatuwezi kuzifikia shule 17,000 peke yetu bila ushirikiano wa wananchi.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona, naomba niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, Shule ya Msingi Majimatitu ina wanafunzi zaidi ya 4,000 hali ambayo husababisha wanafunzi wasipate haki yao ya msingi kitaaluma. Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka kuhakikisha shule hii inaongezewa madarasa pamoja na kwamba amesema kuna shule nyingi zinaongezewa madarasa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, shule ambazo zina wanafunzi zaidi ya 1,500 ni shule ambazo kwa kweli zimezidiwa na wanafunzi wanaohitajika kuwa katika shule moja. Kwa maana kwa viwango ambavyo vinakubalika shule ikiwa na wanafunzi 4,000 kwa kweli ni suala ambalo linahitaji tulishughulikie haraka sana. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Kikwete na wadau wengine wote wa hii Shule ya Msingi Majimatitu kama kweli ina wanafunzi 4,000 basi tutapeleka jicho letu haraka sana ikiwezekana basi tuigawanye ile shule ziwe shule mbili. Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Naibu Waziri wangu kwa majibu mazuri sana ya awali.
Mheshimiwa Spika, nilitaka kuongezea tu kidogo, ni kweli shule ya Msingi Majimatitu mwaka jana darasa la kwanza peke yake walikuwa wanafunzi 1,200 na hii ni kutokana na programu ya elimu bure ambapo watoto wengi waliokuwa wanakosa fursa ya elimu wameenda pale. Serikali tulichokifanya ni kutafuta eneo lingine kwa ajili ya kujenga shule pacha jirani. Naomba niseme kwamba Serikali itafanya kila liwezekanalo ili ile shule pacha iweze kukamilika haraka iwezekanavyo tupunguze idadi ya wanafunzi walioko katika Shule ya Msingi Majimatitu.
MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Spika, Shule ya Msingi Iputi iliyoko Kijiji cha Mbunga katika Jimbo langu la Ulanga ina msongamano mkubwa sana wa wanafunzi. Sisi tumejenga wenyewe shule nyingine, tumejenga ofisi ya mwalimu kwa kushirikiana na Mbunge wao, tunachoomba usajili na kutuletea walimu. Je, Serikali ipo tayari? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA TAWALA ZA MIKOA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godluck Mlinga, Mbunge wa Ulanga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ametupa habari hapa Bungeni kuhusu Shule ya Msingi Iputi ambayo tayari wananchi kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wao wameshaanza ujenzi wa miundombinu ya shule hiyo katika Kijiji cha Mbuga. Nataka nimhakikishie kwamba, naomba ushirikiano wake tukitoka hapa Bungeni leo tuwasiliane na wenzetu wa Wizara ya Elimu ili shule ile tuanze taratibu za kuisajili na tukishaisajili tutaipatia walimu. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri aliyotoa Naibu Waziri, nina maswali mwili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, katika jitihada hizo za kuimarisha maeneo yaliyokuwepo sasa kuna tatizo la Watendaji Kata maeneo mengi katika Jimbo la Tunduru Kusini na Tunduru kwa ujumla walio wengi wanakaimu.
Je, Serikali itapeleka lini watendaji wa kudumu ambao wameajiriwa katika nafasi ya Kata, Vijiji na Katibu Tarafa?
Swali la pili, kwa kuwa majukumu mengi yaliyopo kwa sasa Vijijini yanafanywa na Watendaji wa Vijiji wakishirikiana pamoja na Wenyeviti wa Vijiji; na kwa kuwa Halmashauri nyingi zimeshindwa kutoa posho kwa maana ya asilimia 20 kwenye Vijiji husika.
Je, Serikali haioni haja kwa sasa kutoa posho kwa viongozi wa vijiji kwa maana ya Wenyeviti wa Vijiji ili waweze kufanya majukumu yao vizuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika nchi tunao upungufu mkubwa wa Watendaji wa Kata, kwa kweli siyo Watendaji wa Kata peke yake bali kada nyingi na Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuhakikisha kwamba tunamaliza au tunapunguza kwa kiasi kikubwa upungufu wa watendaji wetu katika kada mbalimbali. Kwa upande wa Watendaji wa Kata, mwaka jana tuliajiri nafasi chache lakini mwaka huu tunao mpango wa kuajiri Watendaji wa Kata 1,000 nchi nzima. Ninaamini watakapoajiriwa hao watapunguza sana upungufu wa uwepo wa Watendaji Kata katika Kata nyingi hapa nchini ikiwemo Kata za Wilaya ya Tunduru.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili kwamba Watendaji wa Vijiji na Wenyeviti wa Vijiji ndiyo wanaofanya kazi kubwa huko kwenye vijiji vyetu. Napenda nikubaliane sana na Mheshimiwa Daimu Mpakate kwamba ni kweli Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Vitongoji wanafanya kazi kubwa kwa kuwaongoza vizuri watendaji wa vijiji walioko huko kufanya kazi za Serikali kwa niaba ya wananchi.
Mheshimiwa Spika, amesema kwamba posho hawapati, natoa hapa agizo ambalo lilishatolewa na Serikali tayari kwamba suala la kushusha asilimia 20 ya mapato ya ndani kupeleka kwenye Kata, Vijiji na Vitongoji kwa ajili ya posho za Waheshimiwa Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji, hilo ni suala la kikanuni na kisheria.
Kwa hiyo Wakurugenzi wa Halmashauri ni lazima watekeleze agizo hilo kikamilifu. Pale ambapo tutagundua kwamba mtu hatekelezi kwa sababu tu ya ujeuri au ukaidi itabidi tuchukue hatua za kiutawala na kiutumishi. Kuna wale ambao ni Wakurugenzi wanapata shida kidogo kutokana na makusanyo hafifu, tunawaomba sana Mabaraza ya Madiwani waridhie mapendekezo ya wataalam kuhusu kupanua wigo wa vyanzo vya mapato ya ndani ambavyo vitasaidia kuweza kupatikana fedha ambazo hatimaye zitapelekwa kwa viongozi hawa kwa ajili ya posho.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imesitisha ugawaji wa maeneo makubwa yakiwemo Majimbo pamoja na Wilaya, lakini kuna Kata moja iko mlimani inaitwa Kata ya Mkanana, hata Mheshimiwa Spika unaifahamu ni milimani hasa. Makao Makuu ya Kata yako kilometa 50 wanateremka kusikiliza mikutano. Je, Serikali inasemaje kuhusu Kata hii ya Mkanana na Chibwegere ili wazigawe? Wananchi wanapata shida sana kusafiri.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, ni kweli kama alivyosema, tumesitisha, lakini kulingana na umuhimu na mahitaji ya muda maalum, kama ambavyo tumepitisha uanzishwaji wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma na kuutangaza Mji wa Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi kwa sababu ni mahitaji maalum kwa muda maalum, kwa suala hili la Kata ya Mtanana kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amelieleza vizuri sana hapa Bungeni na kwa sababu anawawakilisha wananchi wake ambao anaamini wanapata shida kwenda kwenye Makao Makuu ya Kata kilometa 50, namuagiza Mkurugenzi wa Serikali za Mitaa kesho aende Mtanana na timu yake ya wataalam ili watuletee mapendekezo yao.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba niishukuru Serikali kwa majibu mazuri, na ni nia ya wananchi kuona kuwa eneo hilo linatengwa na kunakuwepo na viwanda ili wananchi wa Mbeya waweze kupata ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo mikakati mizuri, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Je, ni lini sasa Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kumalizia Kiwanda cha Kuchakata Nyama ambacho kimejengwa na Halmashauri ya Mbeya na ambacho vyombo vyote, vifaa vyote zaidi ya miaka miwili sasa viko mle ndani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa vile kuna wafugaji wengi katika Kata ya Mjele na tatizo lao kubwa ni mabwawa ya maji, je, ni lini Serikali sasa itapeleka miundombinu ya mabwawa ya maji kwa ajili ya mifugo na binadamu? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru kwamba amekubaliana na majibu ya Serikali kwenye swali la msingi na katika maswali yake mawili ya nyongeza, la kwanza, kuhusu mradi wa kiwanda cha kusindika nyama pale Mbalizi ambao uliwasilishwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya Vijijini TAMISEMI kwa ajili ya kufikiriwa kupewa fedha ni miongoni mwa miradi ya kimkakati katika halmashauri hiyo ambayo imeombewa fedha kwenye dirisha maalum la miradi ambayo ni miradi ya kibiashara.
Kwa hiyo, mchakato wake bado unaendelea, kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha miradi hiyo yote bado inafanyiwa upembuzi maalum ili utakapokamilika miradi ile ambayo itapatiwa fedha wahusika wa Halmashauri wataarifiwa. Hata hivyo ninaamini mradi huo ni mzuri na una faida na miradi kama hiyo Mbeya haipo mingi, kwa hiyo, ninaamini utapewa kipaumbele unaostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kuhusu bwawa kwenye eneo la wafugaji. Najua Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi alitembelea eneo hilo na akatoa ahadi. Mimi nataka nimwambie kwamba Serikali hii ni moja, nitafuatilia mimi mwenyewe kwa Wizara ya Mifugo ili kuhakikisha kwamba Halmashauri na wakazi wa eneo hilo wafugaji wanapata kile ambacho Mheshimiwa Naibu Waziri alikiahidi. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo yaliyoko huko Mbalizi yanafanana kabisa na yaliyoko katika Halmashauri ya Itigi ambapo shamba la Tanganyika Packers eka 45,000 ambalo lipo pale kwa miaka mingi limetelekezwa na Serikali imekuwa na kauli tata juu ya shamba hili wakati tukiliomba lirudishwe kwa wananchi au kuanzishwe mradi mwingine, kwamba litarudishwa, baadae Serikali inasema italichukua. Sasa nini kauli sahihi ya Serikali kwa shamba la Tanganyika Packers ambalo limeachwa na limetelekezwa kwa muda mrefu katika Halmashauri ya Itigi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nisisitize kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kwamba maeneo kama lile la Tanganyika Packers Mbeya na maeneo mengine ya aina hiyo Serikali haina nia ya kubadilisha matumizi ya msingi yaliyokusudiwa kwa ajili ya kuendeleza maeneo hayo katika sekta ya viwanda.
Kwa hiyo, maeneo hayo ni lazima yaendelee kutengwa na kutunzwa kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya viwanda. Kwa hiyo, maeneo hayo ni ya uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ndugu yangu Mheshimiwa Yahaya naomba tushirikiane na Halmashauri ya Wilaya ya Itigi kuhakikisha kwamba eneo hilo linaendelea kulindwa na miongoni mwa maeneo ambayo ni ya halmashauri ya wilaya ambayo mnatakiwa myalinde kikamilifu kwa ajili ya sekta ya viwanda na uwekezaji kwa ujumla ni eneo hilo, kwa hiyo, naomba sana tushirikiane katika hilo.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu linakuja kwenye haya mashamba. Katika Jimbo la Mlimba, Kata ya Namwawala, Vijiji vya Idandu, Miomboni na Namwawala sasa hivi kuna hekaheka kubwa kuzuia wananchi kwenda kulima mashamba yaliyokuwa eneo la Ramsar na matokeo yake na huku kijijini kwenyewe wanasema kuna uwekezaji wa sukari, lakini mpaka sasa Serikali hawasemi chochote kuhusu wananchi hao na Waziri Mkuu anajua, aliniahidi atakuja kutatua hiyo migogoro ili wananchi wawe kama outgrowers.
Je, lini sasa Waziri atakwenda Jimbo la Mlimba katika maeneo haya kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanapata mahali salama pa kulima na pa kuishi katika Kata ya Namwawala na Mofu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema yeye mwenyewe, maeneo ambayo ni mashamba halafu hapohapo akataja jambo kubwa kabisa katika mazingira duniani linaitwa Ramsar, maeneo ambayo yametengwa kama Ramsar Sites ni maeneo ambayo hayastahili kuvamiwa au kutumiwa kwa maendeleo ya aina yoyote, yanatakiwa kulindwa, kuhifadhiwa kwa ajili ya mazingira. Mimi nadhani suala hili tutaendelea kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira kuhakikisha kwamba maeneo hayo yanatunzwa vizuri. Ahsante sana. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuongeza katika majibu mazuri kabisa yaliyotolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Ni sahihi kabisa kwamba uhai wa ikolojia ya Mto Rufiji unategemea sana afya ya maeneo haya yaliyohifadhiwa kwa mujibu wa Mkataba wa Kimataifa wa Ramsar. Kwa hiyo matumizi ya maeneo yale lazima yawe uangalifu na Serikali kabla ya kuruhusu kazi za kilimo, ufugaji na matumizi ya kibinadamu, lazima ifanye utafiti wa kutosha na wa kujiridhisha ili tusije tukaharibu mifumo ya ki-ikolojia ya nchi yetu kwa kuruhusu shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ambayo hayastahili kabisa kufanyika shughuli hizo.
MHE. KANALI MST. MASOUD ALI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, tatizo la ombaomba lina muda mrefu na limekuwa likishughulikiwa na Serikali na likiulizwa mara kwa mara lakini bado ombaomba wanaonekana wakirudi mitaani. Je, ni hatua gani madhuhuti sasa Serikali imeziweka ili hao ombaomba wasirudi tena?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kweli kama alivyosema Naibu Waziri, wakamatwe na washtakiwe, lakini je, hawa hawafanyi kwa makusudi, wanafanya kutokana na hali ngumu ya maisha. Je, wanapotoka huko gerezani baada ya kuwafunga na vitu vingine, hatua gani za Serikali zinachukuliwa kuwasaidia kimaisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, hatua ambazo Serikali inazichukua ni kutoa fursa kwa wananchi wote ili waweze kuzitumia kwa ajili ya kujikomboa kiuchumi na kupambana na umaskini. Hatua hizo nimezitaja kwenye jibu la msingi kama vile kutoa fursa mbalimbali za mikopo, kuwepo kwa ardhi ya kutosha yenye rutuba na vilevile kuwa na programu nyingi za kuboresha huduma mbalimbali katika maeneo ya vijijini ili watu wasitoke vijijini wakaja mijini kufuata huduma hizo. Kwa hiyo, hiyo ni mojawapo ya hatua madhubuti lakini hii hatua ya kuwakamata na kuwarudisha makwao imeonekana ni kama vile haisaidii sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili, hali ya maisha ni ngumu ni kweli na ndiyo maana nimesema kwamba tutumie hizo fursa. Kwa kusema ukweli fursa ya Elimu Msingi Bila Malipo ni muhimu sana tuifuatilie vizuri ili watoto wetu wote ambao wanastahili kuwa shuleni wawe shuleni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombaomba wengi wamekuwa wanatumia watoto ambao wanatakiwa kuwa shuleni na wanazagaa hovyo mitaani, ndiyo maana nikatoa wito kwamba Sheria ile ya Elimu na Kanuni ya Adhabu itumike kikamilifu katika kuhakikisha kwanza watoto wote warudishwe shuleni na vilevile wazazi ambao hawatekelezi wajibu wao nao vilevile wachukuliwe hatua za kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hali ngumu ya maisha, fursa ziko nyingi, naomba sana zitumike ili kujikomboa na hali ngumu ya maisha.
MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, amezungumza kwamba sababu nyingine inayochangia ni pamoja na imani za kidini na hali ngumu ya maisha. Ni kwa nini sasa Serikali isichukue jukumu la makusudi, kwa sababu tatizo la ombaomba kwa watu wengi ni mindset, la kuelimisha jamii kwa vipindi mbalimbali vya redio na television kuhakikisha tunabadilisha mtazamo kusudi hawa watu kama ni imani za kidini waende kwenye imani wanazoziamini wakapate misaada huko badala ya kuwa barabarani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wake ni mzuri na yeye ni kiongozi wa dini. Nadhani sababu mojawapo ya kuwepo kwa ombaomba wengi kama nilivyosema kwenye jibu la msingi ni kwamba watu wengine wanatoa misaada kama sehemu ya ibada. Ndiyo maana unakuta ombaomba wengi siku kama za Ijumaa na Jumapili wanakuwa wengi zaidi katika maeneo hayo ambayo ni ya ibada ni kwa sababu watu wengine wanatoa fedha kama misaada. Kwa hiyo, kwa kweli kama ushauri wake ulivyotolewa tunauchukua kwa ajili ya kuupangia bajeti ya kutoa elimu kwa umma ili kusudi kupunguza hili tatizo la ombaomba.
MHE. SAADA MKUYA SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mheshimiwa Naibu Waziri katika majibu yake ya msingi fursa ambazo amezionesha ni pamoja na mikopo lakini tunajua kiukweli wale ombaomba hawana asset yoyote na taasisi zetu za kifedha mara nyingi zinahitaji at least uwe na asset au uwe na jambo linguine.
Sasa Serikali haioni umuhimu wa kupanga mkakati maalum specifically kwa ajili ya hawa ombaomba ili waondokane na hii hali waliyokuwanayo rather than ku- generalise wapate mikopo ambayo sio rahisi kiukweli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema kwamba taasisi nyingi za kifedha zinadai collateral ili watu wapate mikopo, lakini kwenye utaratibu wetu wa Serikali kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ambayo tumeipitisha mwaka huu hapa Bungeni ni kwamba, mtu atapata mkopo kutokana na shughuli anayofanya. Ndiyo maana nimetoa wito kwamba watumie fursa ya ardhi yenye rutuba kuzalisha mali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama hawa ombaomba watapata elimu nzuri kupitia halmashauri zao, Maafisa Maendeleo ya Jamii watoe elimu hiyo, wakajiunga kwenye vikundi vya uzalishaji mali wanayo fursa ya kupata mikopo kupitia halmashauri, ile 10% ambapo 4% inakwenda kwa vijana 4% inaenda kwa wanawake na 2% inaenda kwa walemavu. Kwa hiyo, hiyo ni fursa mojawapo ambayo ni nzuri ya kupata mkopo bila kuwa na collateral au kuwa na asset yoyote. Jambo la muhimu sana ni Maafisa Maendeleo ya Jamii na Maafisa Ustawi wa Jamii watumike kuelimisha wananchi ili watumie fursa zilizopo.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru Serikali kwa majibu yake mazuri. Kwa kuwa hawa Makatibu Wasaidizi wa Tume wote hawajawahi kuteuliwa na hawatambuliki kisheria.
Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwateuwa hawa ili waweze kufanya kazi yao ipasavyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa mashauri mengi ya walimu yamekaa kwa muda mrefu kwa sababu ya ukosefu wa fedha na fedha nyingi haziendi, na leo Serikali imekiri imetenga shilingi bilioni 4.6; Mheshimiwa Waziri anawahakikishiaje viongozi hawa kwamba fedha hizi zitaenda kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama nilivyosema katika swali la kwanza kuhusu uteuzi. Uteuzi huwa ni hatua ya mwisho ya mchakato, na mchakato wenyewe huanza na upekuzi, kumpekua yule mtu unayempendekeza kwenye nafasi fulani. Kwa hiyo mchakato huo uko katika hatua za mwisho.
Napenda kulithibitishia Bunge hili na Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato huo wa upekuzi ambao Idara ambazo zinazofanya upekuzi anazifahamu Mheshimiwa Mbunge zitakapokamilisha upekuzi huo, Makatibu Wasaidizi wote katika Wilaya watateuliwa kwa mujibu wa mapendekezo ya huo upekuzi utakapokamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili naomba nimhakikishie kwamba wakati wa mazungumzo yetu wakati wa bajeti tumehakikishiwa na Waziri wa Fedha kwamba kwa mwaka ujao wa fedha, fedha hizi zitatoka kwa wakati. Ahsante sana.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwa kuwa hivi sasa mashtaka mengi ya walimu yanachukua muda mrefu na kwa kuwa walimu hawa wanalipwa mishahara na kitendo kinachofanya wasitoe mchango wao.
Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kutoa waraka au maelekezo ya mashtaka haya kuchukua muda mfupi ili walimu warudi kwenye masuala yao ya utumishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna baadhi ya maeneo kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge mashauri yamechukua muda mrefu. Hata hivyo utaratibu mwingine unaosababisha mashauri kuchukua muda mrefu ni kwa sababu kutakuwa na baadhi ya mambo ambayo yanahitajika katika huo mchakato wenyewe wa kusikiliza hayo mashauri. Mimi napenda niungane naye, kwamba tutatoa maelekezo hivi karibuni; kwa mashauri ambayo yako shuleni ambayo hayahitaji gharama kubwa na yako chini ya Mwalimu Mkuu wa shule yaweze kusikilizwa haraka iwezekavyo. Mashauri ambayo yako kwenye halmashauri ya wilaya au katika wilaya kwa Katibu Msaidizi tutatoa maelekezo hivi karibuni ili kusudi kasi yake iweze kuongezeka ya kusikiliza.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Mimi nataka kujua kutoka Serikalini ni lini Walimu waliohamishwa kutoka shule za sekondari kwenda shule za msingi watalipwa stahiki zao. Kule Karagwe kuna walimu 131 mpaka hivi sasa wanasubiri stahiki zao. Serikali ilitoa shilingi milioni 52 na hela ambayo inayohitajika ni shilingi milioni 430. Sasa nataka kusikia kutoka Serikalini, walimu hawa mnawaambia nini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kusisitiza kauli ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa kuanzia mwezi wa pili kwamba uhamishaji wa watumishi usifanyike hadi pale kunapokuwa na fedha za kuwalipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kuna walimu ambao walikuwa tayari wakati huo tamko linatolewa walikuwa wameshahamishwa na ni wengi sio wachache; na kwa sababu walikuwa wameshahamishwa haiwezekani tena kuwarudisha kwenye vituo vyao vya zamani kwa sababu tayari wameshahama na wengine tayari walikuwa wameshapewa baadhi ya fedha na Halmashauri kwa ajili ya kujikimu. Sisi tunawaomba walimu wote wenye stahiki za kulipwa stahili basi waweze kuwa na subira unapoanza mwaka ujao wa fedha kwa bajeti mpya tutahakikisha wamelipwa stahili zao.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri wa TAMISEMI, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa eneo la Sasawala ndiyo eneo ambalo linategemewa kuanzisha Wilaya Mpya na Makao Makuu yake kuwa Lusewa; je, ni kwa nini Serikali isianzishe Jimbo jipya la Uchaguzi katika eneo hilo la Sasawala?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ilifuata utaratibu wote wa kuanzisha Wilaya mbili, kwa maana Wilaya ya Tunduru Kusini na Tunduru iliyopo sasa na kwa kuwa Halmashauri hiyo iliendesha vikao vya kuanzisha miji midogo miwili, katika Vijiji vya Nalasi na Mchoteka; je, Serikali haioni haja kwa sasa kuanzisha miji midogo katika eneo la Nalasi na Mchoteka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu yangu katika maswali yake mawili ya nyongeza, hayawezi kutofautiana sana na jibu langu la swali la msingi. Kuhusu kuanzisha Jimbo jipya, utaratibu wake uko tofauti kidogo na utaratibu wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuanzisha Jimbo jipya linahusisha sana Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi kabla ya michakato yoyote ya mikutano haijaanza, inatakiwa itangaze nia ya kuanzisha Jimbo jipya katika eneo fulani, baada ya hapo ndiyo vikao viridhie na baadae Mheshimiwa Rais aridhie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kwamba michakato ya kuanzisha Wilaya mbili kutoka katika Wilaya moja ya Tunduru, kwa maana Tunduru na Tunduru Kusini na miji aliyoitaja kwamba iwe miji midogo, utaratibu wake ni sawasawa na jibu langu kwenye swali la msingi kwamba hii miji midogo ni maeneo mapya ya utawala, kwa maana kwamba ukishakuwa na mji mdogo utakuwa na Halmashauri ya Mji, Mkurugenzi na utakuwa na vikao vinavyohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, maeneo hayo yote ya utawala yamesitishiwa kuanzishwa hadi hapo tutakapoimarisha zaidi maeneo tuliyonayo sasa hivi. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Jimbo la Mpanda Vijijini ni kubwa lenye kilometa za mraba 16,900. Jimbo hili limekuwa vigumu sana kurahisisha shughuli za kiutendaji kwa sababu ya ukubwa.
Je, ni lini Serikali itafikiria kuligawa Jimbo hili ili kupeleka huduma kwa wananchi kuwa karibu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba hapa nchini yako maeneo ambako Majimbo yake ni makubwa sana pamoja na hili Jimbo ambalo Mheshimiwa Kakoso amelitaja.
Sasa utaratibu wake hautofautiani sana na maelezo ambayo nimeyatoa hapo awali kwamba namuomba Mheshimiwa Mbunge tushirikiane, lakini hasa yeye kuwasiliana na Tume ya Taifa ya Uchaguzi ili waingize kwenye orodha ya maeneo ambayo watayataja kwamba yanahitajika kugawanywa kuwa Majimbo mawili. Kwa hiyo, naomba sana tushirikiane baada ya hapa pengine tuonane ili tupeane maelezo zaidi.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kusini unaozungumzwa ilikuwa uchangiwe pamoja na Wilaya ya Liwale, Nachingwea na Masasi kutokana na mikoa hii kuwa mbali na Makao Makuu ya Mikoa. Serikali kusitisha uanzishwaji wa Mkoa huu wa Selous, huoni kwamba ni kuwanyima haki ya kimsingi wananchi wanaokaa maeneo haya ambao wako mbali sana na Makao Makuu ya Mkoa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza katika swali lake ameongeza maeneo ambayo hayajawahi kujadiliwa; yapo maeneo aliyoyaongeza hapa kama Liwale na wengine wanazungumza Nanyumbu kwamba iwe katika sehemu ya Mkoa mpya wa Selous.
Katika majadiliano yaliyofanyika, maeneo hayo hayakutajwa kwamba ni sehemu ya mapendekezo ya Mkoa mpya. Sasa kwa sababu ni mapya basi naomba sana Mheshimiwa Kuchauka ayapeleke kwenye Mkoa wake wa Mtwara ili waweze kuyajadili kuanzia huko. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa na mimi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuuliza swali, naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kugawa tablets kwa walimu wakuu wa shule za msingi ili kuboresha elimu na ufundishaji. Mheshimiwa Rais aliahidi na ameanza kutekeleza, angalau ni kawaida yake kuahidi na kutekeleza, tunampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa taratibu zote za kuugawa Mkoa wa Tabora zilishakamilika na Serikali iliahidi kutimiza kuugawa mkoa huo ambao una Wilaya saba na una wakazi wengi na kuwasababishia wakazi wa mkoa huo kukosa huduma za msingi kama inavyostahili.
Je, ni lini sasa Serikali itaugawa Mkoa Tabora kama ilivyogawa Mkoa wa Mbeya kuwa Songwe na kama ilivyogawa Shinyanga na Simiyu ili wananchi wa Tabora nao waweze kupata haki zao za msingi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe maelezo kwamba sisi katika Mkoa wa Tabora tunajivunia sana utendaji kazi wa Mheshimiwa Munde Tambwe Abdallah kwa jinsi ambavyo anafuatilia masuala mbalimbali kwenye Mkoa wa Tabora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimkumbushe kwamba Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipotembelea Mkoa wa Tabora mwaka 2017 na kufanya mkutano wa hadhara pale Nzega lilijitokeza swali hili la ombi la kuugawa Mkoa wa Tabora kwamba tuwe na Mkoa mpya wa Nzega.
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu yake katika mkutano ule ndiyo ambayo yamejenga mwongozo wa kitaifa kwa sasa kwamba kuna haja kwanza kuimairisha miundombinu na mahitaji mengine katika Mikoa, Wilaya na Halmashauri mpya ambazo zilishaanzishwa tangu zamani ili tukikamilisha uimarishaji huo ndiyo tuje kwenye mikoa mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mkoa wa Nzega limeshajadiliwa RCC na vikao vyote vimekamilika, tutakapokuwa tumeimarisha maeneo haya mapya yaliyopo, Mkoa huo mpya wa Nzega, naomba sana watu wa Nzega wasiendelee kubishana tena, utatangazwa mara moja na utapewa kipaumbele.
MHE. ALHAJ ABDALAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Swali la kwanza, kwa kuwa suala la madawati limekuwa ni tatizo la muda mrefu na historia iko wazi, kila mtoto akianza shule anaenda na madawati, madawati hayo huwa yanaenda wapi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali ina mkakati gani wa kuweza kuyatunza yale madawati yanapokuwepo shuleni ili angalau na wengine wanaokuja waweze kuyakuta ili ugonjwa wa madawati uweze kuisha katika nchi hii?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Alhaj Abdalah Bulembo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, inashangaza kama yeye mwenyewe ambavyo ameonesha kushangaa kwamba shule inatengenezewa madawati ya kutosha halafu baada ya muda mfupi au baada ya muda baadhi ya madawati yanaonekana hayapo. Mimi nisisitize kwamba ni jukumu la msingi la Mkuu wa Shule au Mwalimu Mkuu kuhakikisha kwamba mali za shule zinatunzwa ipasavyo na tutalifuatilia hili. Kuanzia sasa hivi tunaiweka katika vigezo vya tathmini ya mwalimu kuhakikisha kwamba vifaa vya shule ikiwemo madawati vinatunzwa kikamilifu.
Mheshimiwa Spika, nadhani na swali lake la pili nakuwa nimeijibu kwa namna hiyo. Ahsante sana.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na jitihada nzuri za Serikali ikiwemo Bunge kuchangia utengenezaji wa madawati katika shule zetu za msingi na sekondari lakini madawati haya katika shule nyingi hayakuzingatia mahitaji ya kundi maalum, yaani watoto wenye ulemavu. Napenda tu kufahamu sasa ni mkakati gani unafanya ili tunapotengeneza au tunapofanya kitu chochote kuzingatia kundi hili maalum kwa sababu watoto wengine hawawezi kukaa hata kwenye hayo madawati ya jumla? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amina Mollel, kwa kumwambia kwamba maoni aliyoyatoa tunachukua kuwa ni ushauri kwa Serikali kwa ajili ya kuufanyia kazi. Ahsante sana.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Spika, kama unavyoona hilo jibu la Serikali, nadhani hili linawagusa Wabunge wote. Ni hivi wameweka vituo vya ufundi, wanafunzi wanakwenda kule wanafundishwa lakini wakimaliza hawapewi cheti hata kimoja. Hivi hii ni halali kweli? Hii ni Tanzania nzima. Je, kwa nini Serikali mnawafanyia hivi watoto wa maskini wa nchi hii? Lini mtaanza kuwapa vyeti? Darasa la saba wanapewa vyeti, kwa nini wanaoenda ufundi hamuwapi vyeti ili waweze kujiendeleza? Kama si dhuluma ni nini kwa watu maskini? Hilo ni swali kwanza, Waheshimiwa Wabunge wote linawahusu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, sawa wamesema hiyo inatiwa LGCD kwa maana ya grants. Bunge zima linajua mwaka huu hamna hata shilingi iliyokwenda na Waziri wa Fedha ameshindwa kujibu. Je, hiyo milioni shilingi 10, shilingi 15 mna uhakika gani itakwenda wakati shilingi bilioni 1.5 Wilaya ya Kilombero mpaka sasa mwaka unakaribia kwisha hawajapeleka hata senti 5. Kwa nini Serikali isiwe na mpango maalum na hii ni nchi ya viwanda kupeleka hizo pesa ili vituo hivi vya Mpanga na Mchombe viendelee kuliko kutegemea hiyo grants? Hakuna kitu hapa, hapa tunadanganyana tu, mimi nataka kujua lini mnapeleka hizo hela?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge wa Mlimba kwamba tuko makini na wasikivu na ndiyo maana katika majibu yangu kwenye swali la msingi nimemwambia tumeupokea ushauri wake kikamilifu kwa ajili ya kuufanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, kwanza, kwa sababu mafunzo haya katika vituo hivi ni mapya. Kweli mtalaa ni wa muda mrefu lakini tulikuwa hatuutumii, tumeanza kuutumia mwaka 2015 kwenye vituo hivi 208, tumepata mafunzo mazuri sana ya kutosha na tutakapoanza kutoa vyeti tutatoa vyeti vyote mpaka kwa wale ambao walisoma kuanzia mwaka 2015. Mwakani tutaanza kutoa vyeti, ndiyo maana nimesema tumechukua ushauri wake kwa ujumla kwa ajili ya kuufanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, mimi sipendi sana kuwa mtabiri kutabiri mwaka 2018/2019 utakuwaje. Nimhakikishie kwamba hizi fedha ambazo tumezitaja katika jibu letu la msingi zitaenda wala asiwe na wasiwasi wowote.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kabla ya maswali yangu niseme jambo moja, kwanza siyo dhambi huyo mzazi kuwa na watoto zaidi ya mmoja ambao baadaye atapata hii huduma kwa sababu naye katika kuwasomesha ili watumikie Taifa hili bila shaka ametoka jasho. Kwa hiyo, kwenye jibu hilo nimeona ni jibu jepesi kwa Serikali. Sasa naenda kwenye maswali yangu ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, sasa hivi tunaenda kwenye E-government hata malipo mbalimbali kiserikali tunafanya kwa njia ya mitandao, teknolojia ya mawasiliano imeendelea kukua kwa kasi. Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wa kufanya walau huo utambuzi ili kuwezesha watumishi ambao wanakutana na matatizo kama haya kupata huduma hiyo? Fikiria mtu amefiwa na mzazi Tunduru ampeleke Karagwe na huyu ndiyo mzaa chema mwenyewe!
Mheshimiwa Spika, swali la pili, hiyo nia njema ya Serikali kuruhusu watumishi waweze kuchangiana wakipata matatizo kama hayo ni jambo jema lakini wakati mwingine, mimi nilikuwa mtumishi wa umma mifuko hiyo ina-burst, je, Serikali iko tayari japo kutenga ruzuku ndogo kuisaidia hiyo mifuko ili watumishi wakipata matatizo kama hayo waweze kupata hiyo huduma kwa wepesi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa kama alivyosema kwenye swali lake la kwanza na yeye namuingiza katika Ibara ya 63(2) na (3) ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba Bunge linaweza likaishauri Serikali. Kwa hiyo, kulingana na maendeleo ya TEKNOHAMA na E- government kama unavyosema upo uwezekano mkubwa sana hapo baadaye tukawa na mfumo madhubuti wenye utambuzi kwamba Bwana Joseph Kakunda ana watoto saba wameajiriwa katika sehemu mbalimbali za Serikali, amefariki Joseph Kakunda basi pengine mtoto wake wa kwanza ndiyo atabeba hilo jukumu la kupewa hayo mafao ya mazishi. Kwa hiyo, inawezekana huko baadaye hili likafanyika, tunachukua mchango wake kama maoni kwa mujibu wa Ibara hiyo ya Katiba.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuweka ruzuku kwenye mfuko. Kwanza, napenda nitoe wito kwamba ni vizuri sana kila mahali pa kazi pakawa na mahusiano mazuri, watumishi wenyewe wakawa na mahusiano mazuri wao kwa wao kwanza, kwa sababu katika baadhi ya maeneo ya kazi Mifuko hii ya Rambirambi iko vizuri sana. Hata hapa Bungeni uko Mfuko wa Faraja lakini si Wabunge wote ni wananchama. Kwa hiyo, mimi natoa wito tuanze sisi kwanza kuonesha mfano Bungeni humu Wabunge wote wawe wanachama wa Mfuko wa Faraja. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile mahali pote pa kazi watumishi wajiunge katika Mifuko ya Faraja hii ya Kufa na Kuzikana ambayo ni muhimu sana. Tunauchukua ushauri tena ushauri wake kwamba baadaye tutafikiria kuweka kifungu kidogo kwa ajili ya kuunga mkono uchangishanaji ambao unafanywa na watumishi. Ahsante.
MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa hoja ya msingi ni wazazi pia kuna suala la wake. Baadhi ya madhehebu ya kidini na makabila yanakuwa na mke zaidi ya mmoja. Kwa kuwa Mfuko wa Bima ya Taifa unatambua mke mmoja, je, Serikali iko tayari kuruhusu watu ambao wana wake zaidi ya mmoja waweze kuingizwa katika Mfuko wa Bima ya Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KAKUNDA):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saed Kubenea, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nadhani katika nchi hii kwa sababu Serikali inatambua kwamba wananchi wake wana dini na baadhi ya dini na mila zinaruhusu mke zaidi ya mmoja, hili amelileta kama mchango wa Mbunge na ushauri kwa Serikali, wacha tulichukue kwa ajili ya kulifanyia kazi zaidi. (Makofi)
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Pia nashukuru kwa kuona hilo kwamba kweli Hospitali ya Wilaya ya Lushoto ina msongamano mkubwa sana.
Je, Serikali haioni sasa kuwa ipo haja ya kumalizia vituo vya afya vilivyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi ambavyo ni Ngwelo, Makanya ambayo ni zahanati inayotakiwa ipandishwe hadhi iwe kituo cha afya, pamoja na Gare ili kupunguza msongamano uliopo katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa x-ray machine iliyopo katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto haina uwezo mkubwa wa kuhudumia watu wengi na hivyo kuzidiwa na kuharibika mara kwa mara na wagonjwa kukosa huduma hiyo muhimu; je, ni lini Serikali itapeleka x-ray machine ya kidijitali katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto na kupunguza usumbufu uliosababishwa na ubovu wa mashine hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shekilindi katika swali lake la kwanza kuhusu kumalizia maboma kwenye vituo vya afya vitatu kikiwemo kimoja ambacho wanataka kukipandisha hadhi; nimwambie tu kwamba Serikali inaunga mkono. Mimi naomba sana katika fedha za ruzuku ambazo tutazipeleka hivi karibuni, Halmashauri iweke kipaumbele kikubwa kwenye hivyo vituo ambavyo Mheshimiwa Mbunge amevitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu x-ray, naomba tuendelee na mawasiliano, mwaka wa fedha mpya unaoanza ili angalau ifikapo mwezi wa kumi tuwe tumeshafanya maendeleo mazuri kwenye upande wa x-ray.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, kutokana na swali namba 424.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja Kijiji cha Chiwale na tulifanya pale uzinduzi wa jengo la mama na mtoto, lakini hata hivyo, Kituo cha Afya cha Chiwale tulipewa ahadi ya gari ambayo hatujajua itatekelezwa lini na sasa hivi kile kituo kimekuwa kikubwa na kinahudumia watu wengi sana wa kata zile kwa sababu Jimbo la Ndanda lina Kituo cha Afya kimoja tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kufahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri: Je, ni nini mpango wao wa kuweza kutusaidia pale kuweza kupata angalau mobile x- ray ili kuwasaidia watu wa jirani? Kwa sababu kwenye Kata zote 16 tuna kituo cha afya kimoja tu, kwa hiyo, ni safari ndefu sana kutoka Chiwale kwenda Masasi kwa ajili ya kwenda kupata huduma za afya kwenye Hospitali ya Wilaya ilipo sasa hivi na wenyewe x-ray yao ni mbovu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwambe amezungumza mambo mawili ndani ya swali moja; amezungumzia ahadi ya gari la wagonjwa; nimwambie kwamba tuendelee na mawasiliano ya karibu ili kusudi hiyo ahadi iweze kutekelezwa, kwa sababu nia ya Serikali ni kutekeleza ahadi zake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili hili la x-ray, na mimi nimwombe sana kwamba pamoja na kuweka kipaumbele cha Halmashauri kwenye bajeti zake kwa mwaka ujao wa fedha katika fedha za ruzuku ambazo mwaka ujao zitapatikana mapema zaidi, kama zisipotosha, basi naomba tuwe na mawasiliano ya karibu na ofisi yetu.
MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, lina vituo vya afya vinne na kati ya vituo hivyo tumeanza kutoa huduma ya theater kwenye kituo kimoja cha Lupembe kwa kupitia fedha za ndani lakini pia michango ya wananchi na Mbunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kukamilisha majengo mengine kwenye kituo hiki na kituo kimojawapo ambacho tumeomba cha Kichiwa, kiweze kupata huduma ya theater na kukamilisha majengo yale ya Lupembe kwa kuwa tumeomba muda mrefu na hatujapata fedha yoyote? Tumekosa shilingi milioni 500, tumekosa shilingi milioni 400 na vituo vyote hivi havina hata gari la wagonjwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kukamilisha majengo, Serikali inatambua kwamba yapo majengo mengi sana ambayo yameanzishwa kwa nguvu za wananchi na vilevile kwa uwezo wa Halmashauri na bado hayajakamilika. Nazidi kutoa wito kwamba naomba sana Halmashauri zote nchini ziweke kipaumbele cha kwanza kabisa kumalizia majengo ambayo yameanzishwa. Pale ambapo fedha yoyote ya ruzuku au fedha ya ndani inapokuwa imepatikana, basi waweke kipaumbele sana kukamilisha majengo. Kuhusu gari la wagonjwa naomba tuendelee kuwasiliana na ofisi yetu ili tuweze kukamilisha kazi hiyo.
MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro imekuwa kwenye ujenzi wa wodi ya wazazi zaidi ya miaka mitano sasa na wodi hiyo haijakamilika na kusababisha gharama za ujenzi kuongezeka. Je, ni lini Serikali itatoa pesa za kutosha kukamilisha wodi hiyo ya wazazi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, napenda nitoe ahadi kwamba tutawasiliana ndani ya Serikali ili tuweze kutimiza matarajio ya Mheshimiwa Mbunge katika Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niipongeze Serikali kwa kazi kubwa ambayo imefanya kusema kweli kwa hiki kituo, kilikuwa ni kituo chakavu sana na kinatumika na watu wengi sana. Tunashukuru sana kwa hizi pesa ambazo mmetuletea na kuanzia sasa hivi ukarabati umeanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wafanyakazi wa sekta hii ni wachache sana, hatuna kabisa manesi, madaktari wala wahudumu kabisa; je, ni lini Serikali itatuletea watumishi katika kituo hiki ha Mwese? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Hospitali ya Manispaa ya Mpanda ndiyo hospitali inayobeba matatizo yote katika Mkoa wetu wa Katavi; je, ni lini Serikali itatuletea Madaktari Bingwa, kwa sababu Hospitali ya Mpanda haina Madaktari Bingwa? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nipokee pongezi zake kwa fedha ambazo tumepeleka Mwese na nimpongeze naye mwenyewe kwa kufanya kazi za Kibunge hasa katika Mkoa wake wa Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la watumishi katika Kituo cha Mwese, napenda nimhakikishie kwamba kwa sababu kituo hakijakamilika, Serikali itaweka kipaumbele katika kutenga watumishi ambapo kituo hicho mara kitakapokamailika tu tutawapeleka mara moja ili waweze kutoa huduma kwa wananchi. Hao watumishi tutawaajiri mwezi Julai, wataanza kazi, wataripoti, lakini kuna watumishi ambao tutawa-retain kwa ajili tu ya Kituo hiki cha Mwese.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kupeleka Madaktari Bingwa katika Hospitali ya Manispaa ya Mpanda, kwanza nilitembelea hospitali ile mwezi Novemba, 2017 hospitali yenyewe tu kwanza inahitaji uangalizi wa karibu kwa maana ya ukarabati na mambo mengine. Nimhakikishie kwamba katika ajira ambazo tunaendelea nazo sasa hivi, kati yetu sisi tuna ajira 6,000 ambazo tunaendelea kuziratibu na Wizara ya Afya ina ajira kati ya 1,800 mpaka 2,000 ambazo wanaendelea kuziratibu, basi tutaweka kipaumbele cha kupeleka Madaktari Bingwa kupitia ajira hizi.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza naishukuru na kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa wanayoifanya baada ya kutoa fedha za kupeleka Kituo cha Afya cha Mwese na Kituo cha Afya cha Mishamo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa jiografia ya Jimbo la Mpanda Vijijini ambalo lipo katika Wilaya ya Tanganyika liko katika mazingira ya mtawanyiko; je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka ambulance ambayo itawasaidia kwenye hivyo vituo vya afya; Kituo cha Afya cha Karema, Kituo cha Afya cha Mwese na Kituo cha Afya cha Mishamo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kutokana na eneo mtawanyiko mkubwa wa Jimbo la Mpanda Vijijini lililopo katika Wilaya ya Tanganyika ambayo ni Wilaya mpya kunahitajika ambulance kutokana na kwamba maeneo yako mbalimbali sana; Mwese, Mishamo na kile kituo kingine ambacho amekitaja. Tutakapopata mgao wa ambaulance ambao utapatikana kabla ya mwezi wa kumi, basi naomba sana tuendelee na mawasiliano ya karibu ili tumpe kipaumbele.
MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Katika ziara ya Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI mwezi Machi, 2017 katika Halmashauri ya Monduli aliahidi kusaidia juhudi za wananchi katika Kituo cha Afya cha Makuyuni. Pamoja na hayo, katika mwaka wa fedha 2017/2018 fedha zote za ruzuku tulielekeza katika ujenzi wa Vituo vya Afya.
Je, ni lini Serikali italeta fedha za CDG katika Halmashauri ya Monduli kwa ajili ya kumalizia Vituo vya Afya Lemuoti, Nalarani, Makuyuni pamoja na Duka Bovu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Mheshimiwa Julius Kalanga awe na mawasiliano ya karibu na Mkurugenzi wa Halmashauri kwa sababu wakati wowote fedha za ruzuku zinaweza zikaingia. Sasa zikiingia waweke kipaumbele kwenye hayo maeneo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa, Serikali imenyang’anya vyanzo vya mapato vya halmashauri lakini pia imeshusha asilimia za mazao hasa ya kibiashara kutoka asilimia 5 mpaka 3, hivyo halmashauri nyingi kushindwa kutoa hii asilimia 10. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kusaidia kuongeza ruzuku katika eneo hili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa, zipo halmashauri ambazo zinategemea mazao ya kilimo pekee, kwa mfano Halmashauri ya Lushoto, Halmashauri ya Handeni na nyinginezo na zipo halmashauri ambazo zina rasilimali kama madini, hivyo mfuko huu unakuwa hauna ulingano kwa maana kwamba yapo maeneo ambayo wanapata mapato makubwa na mengine wanapata mapato kidogo sana. Hatuoni kwamba kwa kufanya hivi tunaleta misingi ya ubaguzi katika pato la Taifa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Shangazi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza amesema kwamba, kuna baadhi ya vyanzo vya mapato halmashauri zimenyang’anywa. Nataka nimhakikishie kwamba, utaratibu wa Serikali ni mzuri. Katika baadhi ya vyanzo ambavyo vimechukuliwa, kwa mfano, vinavyokusanywa na TRA, bajeti ya halmashauri inakuwa iko palepale na baada ya ukusanyaji bajeti ambayo ilitengwa huwa inarudishwa kwa halmashauri. Kuhusu kwamba kwa nini tusiweke ruzuku maalum ili kufidia, nadhani ni wazo ambalo tunaweza tukalifanyia kazi kwa mwaka ujao wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili kwamba baadhi ya halmashauri mapato ni kidogo ukilinganisha na halmashauri nyingine. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Shangazi na Waheshimiwa Wabunge kwamba katika ukokotoaji ambao tutaufanya hivi karibuni, kama sehemu ya kuweka utaratibu mzuri zaidi wa kuziangalia hizi halmashauri zetu. Tutaangalia utaratibu ambao ni mzuri zaidi ili kusudi halmashauri ambazo zina uwezo mkubwa na halmashauri ambazo hazina uwezo kabisa tuangalie namna ya kutekeleza agizo hilo.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na taarifa mbalimbali kuhusu baadhi ya halmashauri kutoa mikopo hii ya vijana na akina mama kwa upendeleo. Serikali imewahi kulifanyia uchunguzi jambo hili na inasema nini kuhusu suala hili kama kweli lipo katika baadhi ya halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ngazi yetu sisi ya Wizara hivi karibuni hatujawahi kupokea malalamiko ambayo ni ya msingi kabisa kutoka katika halmashauri yoyote, kwamba kuna upendeleo katika utoaji wa mikopo. Kwa sababu utaratibu uliopo kila halmashauri inatakiwa iwe na Kamati ya Mikopo ambayo ndiyo hupitisha mikopo ile na miongoni mwa Wajumbe wa Kamati ya Mikopo ni Waheshimiwa Madiwani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nijibu tu kwamba, kwa kweli utaratibu uliopo inawezekana kuna baadhi ya vikundi vikawa havijaguswa kwa mwaka ule husika kwa sababu fedha zenyewe zinakuwa hazitoshi, ni kidogo. Kwa mfano, unaweza ukawa na shilingi bilioni moja ukataka kutoa mikopo kwa vikundi 80 katika halmashauri, lakini halmashauri ina vikundi 600 kwa hiyo ni wazi kwamba kuna baadhi ya vikundi vitakosa. Kwa hiyo, jambo la msingi ambalo nataka nishauri halmashauri ni kwamba wasirudie kuvipa mikopo vikundi ambavyo vilipata mikopo mwaka jana na mwaka huu vikapata, bali vipate ambavyo mwaka jana havikupata. Huo ndiyo utaratibu mzuri zaidi na hiyo ni kupitia Kamati ya Mikopo ya Halmashauri.
MHE. KABWE Z. R. ZITTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji ilipitisha Sheria Ndogo ya Nyongeza ya Tozo mbalimbali katika Halmashauri na sheria ile ikasainiwa na Waziri mwenye dhamana wa TAMISEMI. Katika hali ya kushangaza, Katibu Mwenezi wa Chama cha Mapinduzi alikuja Kigoma Machi, 2018 na kutangaza kwamba sheria ile isitekelezwe. Mpaka sasa watendaji wa halmashauri wanaogopa kukusanya ushuru kwa sababu ya agizo la Katibu Mwenezi wa Chama cha Mapinduzi. Serikali inasema nini kuhusu jambo hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kabwe Zuberi Zitto, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ambazo tunazo katika Ofisi ya Rais – TAMISEMI ni kwamba Baraza la Madiwani lilipitisha viwango vya tozo kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, hizo taarifa ndizo tulizonazo na hata Mkuu wa Wilaya ya Kigoma anazo taarifa hio na ametuarifu. Kwa hiyo, hizi taarifa ambazo Mheshimiwa Zitto amezileta ni mpya na yeye ni rafiki yangu, hajawahi hata kuja ofisini kuniambia. Kwa hiyo, tutafuatilia baada ya kuwa amezitoa hapa ili tuone zina ukweli kiasi gani.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami napenda tu kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa halmashauri nyingi kwa sasa hivi ziko taabani, kwa maana kwamba kimapato nyingi zinasuasua; na kwa kuwa Serikali imeendelea kuchukua baadhi ya vyanzo vingi vya halmashauri na hivyo kufanya halmashauri hizi kushindwa kufanya kazi na kutekeleza majukumu yake kama ilivyotakiwa. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaamini kwamba kwa mwenendo huu unazidi kuuwa ile dhana ya kugatua madaraka ya D-by-D?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Chegeni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza jukumu la msingi kubwa la Serikali ni kusimamia maendeleo ya wananchi wake wote kwa usawa. Kuna baadhi ya halmashauri unaweza ukakuta katika maeneo yao kuna vyanzo ambavyo vinaweza vikawa vinawapatia mapato ambayo kimsingi yakikusanywa kwa asilimia 80 hadi asilimia 100 yanaweza yakatoa mchango mkubwa sana katika pato la Taifa ili kuweza kuligawanya na halmashauri nyingine ambazo zina matatizo ziweze kupata japo kidogo. Kwa hiyo, huo ndiyo msingi wa baadhi ya kodi kuweza kuchukuliwa kukusanywa na TRA ili kusudi ule mgawanyo wa mapato kitaifa uweze kuwa mzuri zaidi kwa halmashauri zote au kwa maeneo yote, hilo ndio jambo la msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, pamoja na changamoto ambazo zipo katika halmashauri jambo la kwanza ambalo tumewashauri na Kamati ya Bunge imetoa ushauri ndani ya Bunge hili ni kwamba, kila halmashauri wakae chini katika vikao vyao vya mabaraza watathmini vyanzo vya mapato walivyonavyo kwa sababu halmashauri nyingi tu vipo vyanzo vya mapato ambavyo hawavikusanyi. Kwa hiyo, watathmini vyanzo vya mapato walivyonavyo na wanavyokusanya walete Mheshimiwa Waziri aweze kuwapitishia ili kusudi waweze kuongeza wigo wa mapato. Ahsante sana.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu ambayo yamewasilishwa hapa Bungeni na Serikali muda huu yanaeleza kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI inatengeneza kanuni za kulazimisha halmashauri iweze kutenga hizo fedha kwa ajili ya mfuko huu. Suala si kuwa na kanuni na sheria kali, suala ni kwamba vyanzo vingi vya halmashauri vimechukuliwa na Serikali Kuu hivyo halmashauri inashindwa kutenga fedha kwa ajili ya kuwapa mikopo wanawake na vijana. Ni kwa nini Serikali sasa, kwanza iache kutengeneza kanuni hizo lakini itenge fedha hizo kutoka kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali kwa sababu mapato yote imeyachukua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Paresso na Bunge lako Tukufu kwamba agizo la kutenga asilimia 10 linahusu makusanyo ya ndani. Kama wamekusanya Sh.100 basi asilimia 10 ya Sh.100 watenge hiyo hiyo. Hatujasema kwamba mtu amekusanya Sh.100 atenge Sh.200, hapana. Amekusanya Sh.100 basi atoe asilimia 10 ya hiyo Sh.100 ili kusudi aweze kutoa mikopo kwa vikundi vya vijana na wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri ambayo imekusanya Sh.100,000,000 inatakiwa itoe Sh.10,000,000 kwa ajili ya vikundi vya vijana na wanawake. Kwa hiyo, kama kuna changamoto nyingine, taratibu za mawasiliano ndani ya Serikali Wakurugenzi wa Halmashauri wanazifahamu sana. Ahsante sana.
MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Kwa vile Naibu Waziri ameona aondoe sentensi moja, mimi nasema paragraph yote majibu hayafanani na swali nililouliza. Mimi sitaki kuuliza maswali mengi, nimwombe tu Mheshimiwa Naibu Waziri au Mawaziri wote watatu wa TAMISEMI wafike Ulyankulu kujionea haya yaliyoandikwa, je ni kweli? Kwa sababu haya yote yaliyoandikwa si kweli.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi nimwombe Naibu Waziri au wenzake waweze kufika Ulyankulu na kujionea kile wanachopewa na wataalam na je, ndicho kilichoko site? Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, naomba sana nimwombe Mheshimiwa John Kadutu, awepo Jimboni tarehe 10 Julai, ili tuweze kutembelea shule hizo kwa pamoja.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, shule za sekondari za kidato cha kwanza mpaka cha nne Serikali imezipandisha hadhi baadhi yake kuwa shule za kidato cha tano na cha sita, kwa mfano, Kibakwe, Berege, Mazae na Kongwa Mjini. Hata hivyo, watoto katika shule hizi wanasoma katika mazingira magumu sana kwanza madarasa, hosteli pamoja na mabweni lakini hata chakula wanachopewa hela ni kidogo sana. Mheshimiwa Naibu Waziri anasemaje kuhusu suala la kuboresha shule za form five na six katika kata hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nichukue nafasi hii kumpongeza, yeye ni Mbunge mzoefu wa siku nyingi na kutokana na Ubunge wake ndiyo maana ameweza kupata maendeleo makubwa katika Jimbo lake hadi shule hizo alizozitaja zimesajiliwa kuwa katika hadhi ya kidato cha tano na sita. Kuwa na shule tatu au nne kwenye Jimbo moja za kidato cha tano na sita siyo kazi ndogo, ni kazi kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika jibu hili, napenda kujibu kwa ujumla kwamba shule zote za kidato cha tano na sita na hata za kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne, zote zinapewa fedha sawasawa kwa nchi nzima. Kwa hiyo, haiwezekani kwa mfano tukasema kwamba, kwa sababu shule hizi sasa Mheshimiwa Mbunge amesema zina matatizo makubwa, basi tuziongezee shule zile za Jimbo lake tu, ni kitu ambacho hakiwezekani. Kwa hiyo, nakaribisha maoni kama haya ili tuweze kuyajadili kwa pamoja kwa ajili ya shule zote nchini badala ya shule moja moja. Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. ALHAJ ABDALLAH M. BULEMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa swali la msingi la Ulyankulu liko katika Majimbo mengi ya nchi hii, kutokuwa na shule za form five na form six. Serikali inatoa commitment gani na lini itaanza kufanya operation katika kila jimbo kupata shule za form five na form six? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, maombi yaliyopo katika Wizara yetu ambayo sisi tukiyapokea tunayapeleka Wizara ya Elimu kwa ajili ya usajili kwa sababu anayesajili ni Wizara ya Elimu ni mengi, lakini mengi yamekuja hivi karibuni, mwezi wa Nne mwishoni, mwezi wa Tano wakati tayari masuala ya bajeti yalikuwa yameshakamilika. Kwa hiyo, naomba sana nimwahidi Mheshimiwa Bulembo pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote na Bunge zima kwamba mwakani tutaweka utaratibu maalum wa kuhakikisha kwamba inavyofika Desemba, 2018, basi shule zote ambazo zina maombi maalum katika ofisi zetu za Serikali tutazisimamia ili ziweze kupata usajili.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nimesimama kulihakikishia Bunge lako Tukufu Wizara yangu ambayo ndiyo ina jukumu la kusajili shule haina tatizo lolote la kusajili wakati wowote shule ambayo imekidhi vigezo. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge na Wakurugenzi na Maafisa Elimu kwa ujumla kama kuna shule ambayo inahitaji usajili, tunasajili wakati wowote ilmradi shule imekidhi vigezo. (Makofi)
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Nataka kuuliza jambo moja kwamba majengo haya ya Serikali yanachukua muda mrefu kukamilika na matokeo yake yanagharimu fedha nyingi zaidi ambapo yangejengwa na kukamilika kwa wakati yangesaidia sana matumizi ya fedha za Serikali kutumika kwa uchache.
Mheshimiwa Spika, sasa pamoja na Serikali na jitihada zake kubwa, ni miaka 10 leo. Mwaka ujao wa fedha Mheshimiwa Waziri anatuahidi kwamba jengo hili litakamilika. Naomba sana tufanye jitihada hiyo ili fedha hizi ziletwe na jengo hili likamilike. Hii itachangia hata ukuaji wa uchumi kwenye lile eneo ambalo Jengo la Mkuu wa Wilaya limejengwa. Nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mabula na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, pamoja na mikoa yote na wilaya zote, tumepitisha hapa Bungeni shilingi bilioni 53 kwa ajili ya kujenga majengo ya Halmashauri na tumepitisha hapa shilingi bilioni 80 kwa ajili ya bajeti za maendeleo ya mikoa. Hizi fedha nataka niwahakikishie kwamba Serikali inaendelea kuwa stable kabisa katika masuala ya ukusanyaji wa fedha, fedha zitapelekwa, wala asiwe na wasiwasi wowote.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa sababu Serikali imeweza kutambua angalau kwamba kuna shilingi milioni 92.4 ambazo Manispaa ya Mtwara Mikindani inadaiwa, kwa maana ya shule za msingi na shule za sekondari. Naomba kuuliza maswali yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Shule ya Sekondari Sabasaba, Raha Leo, Chikongola na Shule zote za Msingi za Manispaa ya Mtwara Mikindani zinadaiwa hizi stationery kabla Serikali haijaanza utaratibu wa kupeleka elimu bure. Siku za nyuma ilikuwa michango inakusanywa kupitia kwa wazazi then zinalipwa stationery hizi ambazo zinatumika katika shule za msingi na sekondari. Ni lini Serikali italeta hizi shilingi bilioni 92.4 kwa ajili ya kulipa kwenye hizi shule ambazo zinadaiwa pale Mtwara Mjini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mkuu wa Shule ya Sekondari na Mwalimu Mkuu wa Shule za Msingi ndiyo wanaobeba haya madeni kama yao, ni declare tu interest nilikuwa Mkuu wa Shule, nafahamu kila Mkuu wa Shule anavyotembea anadaiwa yeye. Je, Serikali inawasaidiaje hawa Wakuu wa Shule za Sekondari na Walimu wa Shule za Msingi ili haya madeni yasionekane kama ni ya kwao yawe ni madeni ya Serikali na Serikali iweze kulipa kwa wakati? Ahsante (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tumekiri kwamba Serikali kweli inadaiwa madeni hayo lakini utaratibu wake bado una mchakato ambapo tunahitaji kuyaangalia kwa undani zaidi madeni hayo. Ndiyo maana tumesema kwanza kuanzia Mwalimu Mkuu ajiridhishe na hayo madeni aandike barua kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kwamba nimeridhika kwamba madeni haya ni halali. Mkurugenzi wa Halmashauri alete tena kwetu tuyaangalie tena baadaye tutapeleka Wizara ya Fedha madeni ambayo tulishajiridhasha tena kwa mara nyingine sisi kwamba hayo ni halali halafu Serikali itaweka utaratibu wake vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili kwamba tunawasaidiaje Wakuu wa Shule, wao wenyewe hasa wale waliokuwepo na Mheshimiwa Nachuma ulikuwepo na wewe umezalisha kumbe hayo madeni. Sasa wewe utakuwa shahidi mzuri vilevile katika kutuhakikishia kwamba madeni hayo ni halali. Kweli kama waajiriwa wetu Walimu Wakuu tumewakabidhi dhamana kubwa kwanza hatutaki waendelee kuzalisha madeni mengine kwa sababu sasa hivi tunapeleka fedha. Atakayezalisha deni lolote kuanzia sasa hivi itakuwa ni wajibu wake kulilipa kwa sababu tunapeleka hela sasa hivi. Kwa hiyo, kwa yale ya zamani tunaandaa huo mchakato kama nilivyokueleza katika swali la kwanza ili kusudi tuweze kuwaondolea huo mzigo wa madai.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Serikali inatoa elimu ya bure kwa ngazi ya shule ya msingi na kwa kuwa wanafunzi walewale ambao wametoka shule ya msingi wanaenaenda sekondari kwa maana ya Form I - Form IV na wanafunzi haohao wanafaulu kwenda high school. Kwa sababu hao watoto walikuwa na mazoea ya kutokulipa ada, sasa wanahangaika mitaani kwa kukosa ada ya kwenda Form V. Je, nini kauli ya Serikali kuwasaidia watoto hawa ambao walipata msaada kutoka shule ya msingi wamefanikiwa kwenda sekondari na sasa wamefaulu kwenda high school na hawana uwezo wa kulipa ada? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwita Waitara, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba maoni kama hayo tumekuwa tukiyapata Serikalini siyo kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge peke yao bali hata kutoka kwa wananchi na NGOs mbalimbali. Hata hivyo niseme kwamba Ilani ya Uchaguzi ya CCM imeelekeza kwamba Serikali iandae utaratibu wa kutoa elimu msingi bila malipo ambayo ni kuanzia shule ya msingi mpaka Form IV. Kadri uwezo wa Serikali utakavyokuwa unavyoendelea kuwa mzuri zaidi inawezekana tukachukua ile Form V na VI na mambo yakiwa mazuri zaidi, Serikali ikavyojizatiti ikawa stable zaidi inawezekana tukatoa elimu bure mpaka chuo kikuu.
MHE. ABDALLAH D.CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa siku za nyuma Serikali ilijenga Vituo vingi vya Walimu (TRC) na kwa kuwa sasa hivi havitumiki kwa kukosa fedha, je, Serikali ina mpango gani wa kutumia sehemu ya fedha za elimu bure kupeleka kwenye Vituo vya Walimu ili ziendeshe semina kwa walimu hao katika maeneo yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Abdallah Chikota kwa jinsi ambavyo anasimamia maendeleo kwenye Jimbo lake la Nanyamba na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla na hata kulisaidia Bunge zima na Wizara yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi napenda nilichukue hili kama sehemu muhimu sana ya mchango wa mawazo mazuri na maoni Serikalini kwa ajili ya kulifanyia kazi. Ahsante.
MHE. OMARY A. BADWEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa lengo la Serikali kutoa fedha hizi katika shule za msingi ni kusaidia uboreshaji wa elimu hiyo na sasa ni takribani zaidi ya miaka miwili fedha hizi zimekuwa zikienda katika shule zetu za msingi na sekondari. Je, sasa Serikali katika utekelezaji wa jukumu hili imepata changamoto gani za matumizi sahihi na kuondoa ubadhirifu katika fedha hizi? Kama zipo changamoto hizo wamechukua hatua gani kutatua na kupunguza changamoto hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Omary Badwel, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama alivyosema kwamba sasa hivi tuna uzoefu wa miaka miwili katika kugharamia elimu msingi bila malipo. Napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya Waziri wangu na Serikali kuwasifu sana wasimamizi wote wa elimu kuanzia Maafisa Elimu katika ngazi ya mkoa, wilaya na halmashauri na Wakaguzi wa Ubora na wasimamizi wa elimu katika ngazi ya kata, Maafisa Elimu wa Kata na Walimu Wakuu wa Shule za Msingi wamejitahidi sana kusimamia vizuri fedha hizi kwa mujibu wa maelekezo ya Serikali. Maeneo machache sana ambayo yamekuwa na matatizo hatua zimechukuliwa na wengine wameshtakiwa kupitia Tume ya Utumishi wa Walimu na wachache sana ambao wameweza kuchukuliwa hatua. Siwezi kuwataja hapa kwa sababu idadi kamili sina lakini ni wachache sana ambao wamechukuliwa hatua. Kwa ujumla kazi ambayo sasa hivi inaendelea nchi nzima ni nzuri sana na wasimamizi wote wa sekta ya elimu wanastahili pongezi.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa elimu ya msingi ni kuanzia elimu ya awali kwa maana chekechea. Kutokana na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya kupeleka fedha kwa kila kichwa cha mtoto kwenye elimu ya msingi, je, haioni sasa ni wakati muafaka wa kutoa fedha hata kwenye hii elimu kwa hawa watoto wa shule za awali ili kusudi ziweze kusaidia katika uendeshaji wa madarasa haya ya awali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mary Chatanda, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia kwamba elimu msingi bila malipo inaanzia madarasa ya awali ambayo ni sehemu ya shule za msingi na shule za sekondari hadi kidato cha nne. Tunapopeleka fedha kwenye kila shule mgawanyo wake umeainisha wanafunzi wote kuanzia madarasa ya awali mpaka la saba, kuanzia kidato cha kwanza hadi kidato cha nne. Kwa hiyo, hakuna mtoto anayeachwa katika elimu msingi bila malipo kuanzia madarasa ya awali. Ahsante sana.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, hali ilivyo Chemba inafanana vilevile na kule Mkinga. Tunaishukuru Serikali katika kipindi hiki imetuwezesha kuanzisha sekondari za kidato cha tano na sita kwa Shule ya Mkinga Leo na Maramba Sekondari. Shule hizi zinakabiliwa na tatizo kubwa sana la maji na kukamilika kwa vyumba vya madarasa na mabweni. Je, nini kauli ya Serikali kuwezesha kukamilika kwa nia njema hii ya kuwa na sekondari za A-Level ili ziweze kutoa elimu stahiki kama walivyokusudia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda sana nimpongeze Mheshimiwa Jumaa Aweso kwa majibu yake mazuri. Pengine hakumalizia tu kwamba Wizara ya Maji na Umwagiliaji inakamilisha mchakato wa mwisho kabisa wa kupata dola milioni 350 ambazo ndani yake kuna programu nzuri sana ya kupeleka huduma za maji katika shule za sekondari na za msingi zote nchini ambazo hazina huduma ya maji, pamoja na hizo alizotaja Mheshimiwa Kitandula, Shule za Maramba ambayo ni shule ya zamani sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimhakikishie kwamba tumeshatoa agizo kwa Wakurugenzi wa Halmashauri wote akiwemo Mkurugenzi wake, kuhakikisha kwamba shule ambazo wamezipangia kwamba zitaombewa kibali ziwe kidato cha tano na sita wanaweka kipaumbele cha haraka ili kusudi miundombinu yake iweze kukamilika, maombi yake yaweze kufikishwa Wizara ya Elimu ili zipate kibali ili angalau mwakani ziweze kuanza kuchukua vijana wa kidato cha tano na sita.
MHE. DAVID E. SILINDE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Tatizo la maji katika shule za sekondari pamoja na shule za misingi lipo Tanzania nzima na nimemsikia Mheshimiwa Naibu Waziri hapa wakati anajibu anasema tatizo hilo litatatuliwa katika shule zote za sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nifahamu jambo hilo litatekelezwa lini kwa kuwa tumeshapitisha bajeti na hakuna fedha yoyote iliyopitishwa kwa ajili ya kupeleka maji katika shule za sekondari. Upi ni mpango ambao utasaidia kupeleka maji shule za sekondari na shule za msingi Tanzania nzima ikiwemo Momba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Silinde, Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kitandula, nimetoa ufafanuzi kwamba tunakamilisha mchakato wa mwisho wa kupata hizi fedha ambao ni mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia, dola milioni 350 si hela ndogo, ni hela ndefu. Kwa hiyo, mchakato huu unaweza ukakamilika vizuri kabisa 2018/2019 na fedha hizo zikaanza kutumika 2019/2020 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba shule zetu zote zinaondolewa matatizo kabisa ya kukosa huduma ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika bajeti ambayo tumeipitisha Bungeni hapa ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji na fedha nyingine chache tulizipitisha katika kasma yetu ya TAMISEMI ambazo zote sasa tutazipeleka Wizara ya Maji ili ziweze kusimamiwa vizuri zaidi, zipo bajeti ambazo si kubwa sana kwa ajili ya kuhakikisha tumepeleka huduma za maji katika baadhi ya shule. Ahsante sana.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda kuongezea kidogo majibu mazuri ambayo yametolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba kupitia Mradi wa SWASH kuna kiasi cha shilingi bilioni 16 ambazo zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya maji shuleni. Kwa hiyo, mimi hiyo naona si hela kidogo, tayari Serikali imeonesha commitment, shilingi bilioni 16 zipo kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya maji shuleni kwa mwaka wa Fedha 2018/2019. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Singida Mjini tumeanza programu ya kupandisha hadhi shule zetu za sekondari kuwa kidato cha tano na sita ikiwemo Shule ya Sekondari ya Mungumaji. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutusaidia kukamilisha programu hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mussa Ramadhan Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nikirejea majibu yangu ya awali ambayo nimeyatoa, kwanza yeye kama mwalimu namsifu kwa juhudi zake za kuendeleza sekta ya elimu katika jimbo lake lakini vilevile kutoa mawazo mazuri kwa ajili ya nchi nzima. Napenda kusisitiza kwamba maagizo ambayo tumeyatoa kwa Wakurugenzi wa Halmashauri ambao wanasimamiwa na Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa ni kwamba kipaumbele lazima waendelee kukiweka katika shule zote ambazo wameziteua kwa ajili ya kuzipandisha hadhi kuwa za kidato cha tano na sita kwa maana hizo zitakuwa ni shule za nchi. Waweke kipaumbele kuhakikisha kwamba miundombinu inayohitajika yote kwa mujibu wa vigezo vilivyotolewa na Wizara ya Elimu inakamilika mapema iwezekanavyo ili kusudi shule hizo ziweze kutusaidia kupokea watoto wengi zaidi au vijana wengi zaidi wa kidato cha tano na sita.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Katika Jimbo langu la Singida Kaskazini tunazo sekondari tatu ambazo zilipandishwa hadhi ikiwepo katika Tarafa ya Mgori Mwanamema, Ilongero pamoja na Mtinku. Shule hizi bado zina changamoto zikiwepo za vitanda, magodoro na kadhalika na zingine zimeshindwa hata kupangiwa wanafunzi katika mwaka huu kwa sababu hazijakidhi vigezo. Je, Serikali itatusaidiaje ili kukamilisha vigezo hivyo na shule hizo zianze kutoa huduma kama ilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA):
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Justin Monko, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, amezitaja shule tatu katika jimbo lake ambazo zimepandishwa hadhi, lakini kati ya shule tatu Shule ya Mwanamema Shein kama ilivyo jina lake ni shule ambayo imeboreshwa kwa kiasi kikubwa na sasa hivi wamepangwa vijana kupelekwa pale. Wengine walikuwa wanakuja ofisini kwangu kusema bwana hii Shule ya Mwanamema Shein sisi hatuitambui tunaomba tuhamishe watoto, nimewaambia hatuwezi kuhamisha watoto pale. Watoto waende wakasome pale Shule ya Mwanamema Shein na watapata elimu nzuri, tumepeleka walimu wazuri pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Monko pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba zile shule ambazo zina usajili wa Wizara ya Elimu lakini zinatakiwa kuongezewa miundombinu kidogo tu ili kusudi ziweze kuchukua vijana wengi zaidi kuliko capacity yao ya sasa hivi, wiki ijayo Wizara ya Fedha itapeleka fedha kwenye hizo shule, kama walikuwa wanakosa bwalo watajengewa bwalo, kama walikuwa wanakosa darasa moja watajengewa darasa moja ili kusudi mpaka mwezi wa nane vijana wa second selection waweze kuripoti shuleni.
MHE. MICHAEL J. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu ya Serikali bado kuna matatizo makubwa sana kwenye utendaji katika ngazi hizi za chini zinazotokana na ama na kutokuelewa wajibu wa kila upande katika kusimamia utendaji kwenye maeneo haya. Je, bado Serikali haioni sababu ya msingi kabisa kutoa elimu pamoja na majibu haya yaliyotolewa bado kuna tatizo kubwa sana kwenye usimamizi hasa nyakati za uchaguzi ambapo kumekuwa na migogoro mingi inayotokana na watendaji wanaosimamia chaguzi hizi kufanya au kutoa maamuzi kulingana na maelekezo yanayokuwa yametolewa na viongozi wa juu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kutokana na migogoro hii, Serikali haioni kwamba kuna sababu ya msingi kabisa kutokana na mapendekezo ya Katiba iliyopendekezwa kuwepo na umuhimu wa kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ili kuondoa kabisa migogoro hii inayotokea nyakati za uchaguzi kwenye ngazi mbalimbali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimhakikishie kwanza uzoefu wangu kwamba kati ya mwaka 1996 mpaka mwaka 2000 mwenyewe nilikuwa Ofisa Mtendaji wa Kata, kwa hiyo nina uzoefu mkubwa na kile ninachokielezea na kata yenyewe ilikuwa ni Kata ya Manzese pale Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, chaguzi za Serikali za Mitaa hufanyika kwa mujibu wa sheria na kama atatokea Msimamizi Msaidizi yeyote akatenda kinyume cha sheria, mdau yeyote anao uhuru wa kulalamika katika vyombo vinavyohusika ikiwemo kulalamika kwa Msimamizi wa Uchaguzi na hatua zimekuwa zikichukuliwa dhidi ya watu ambao wanatenda kinyume cha utaratibu wa sheria ya uchaguzi ule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, ameuliza kwamba kuna mapendekezo kwenye Katiba iliyopendekezwa. Sasa kwa sababu Katiba iliyopendekezwa bado hatua zake hazijakamilika, nashauri Bunge lako Tukufu kwamba tusiwahishe mambo, tusubiri kwanza huo mjadala wa Katiba Mpya Iliyopendekezwa ukamilike na mambo yaingizwe kwenye sheria basi hapo tutatekeleza baada ya sheria kuwa imekamilika.
MHE. ZITTO R. Z. KABWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria za Serikali za Mitaa ni pamoja na sheria zinazohusiana na mabadiliko ya Sheria Ndogo za Tozo na Ushuru mbalimbali. Mpaka hapo tunapozungumza, Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji haikusanyi ushuru, watendaji wamegoma kwa sababu ya amri ya Katibu Mwenezi wa Chama cha Mapinduzi. Mara ya mwisho nilivyouliza Waziri alisema hana taarifa na nina uhakika sasa ana taarifa. Anatuambia nini kuhusiana na kutotekelezwa kwa sheria ambayo imetungwa na Baraza la Madiwani na imepitishwa na Waziri mwenye dhamana ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA - (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hoja ambayo ameileza Bunge lako tukufu kwa sasa naielewa vizuri sana baada ya kuwa ameigusia wiki iliyopita. Niseme tu kwamba Baraza la Madiwani la Manispaa ya Kigoma ambalo linaongozwa na ACT lilipandisha ushuru kutoka Sh.15,000 mpaka Sh.50,000 kama tozo kwa wafanyabiashara na hizo ni tozo halali ambazo zinatakiwa kukusanywa na sisi tulimuagiza Mkuu wa Wilaya asimamie tozo hizo ziendelee kukusanywa kama zilivyopitishwa na Baraza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wananchi wa Kigoma wamekuwa wakilalamika na malalamiko yao mengine wameyapeleka kwa viongozi mbalimbali wakiwemo viongozi wa Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, sisi kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tumetuma timu ya watalaam kwenda Kigoma kuangalia kinachoendelea na taarifa yao hawajatuletea. Kwa hiyo, naamini wakituletea taarifa yao Mheshimiwa Zitto Zuberi Kabwe tutampa majibu sahihi zaidi.
MHE. ISSA A. MANGUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali inasema kwamba wameingiza Teaching Allowance katika mishaharana Serikali ilikuwa inafanya uhakiki kwa ajili ya kulipa madeni ya walimu na malimbikizo yao wakati wa kustaafu na wale ambao wako kazini. Je, Serikali imefikia wapi katika kuhakiki madeni hayo na kuyathibitisha ili walimu sasa waanze kulipwa maana wamekuwa wakisumbuka na muda mrefu wamekosa kupata haki zao hasa wale waliostaafu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, anasema kwamba walimu wa mijini wanaweza wakapanga nyumba. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwaongezea allowance hizi ili waweze kukabiliana na changamoto ya nyumba katika maeneo ya mijini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba Serikali imeshakamilisha uhakiki wa madeni na watumishi wengi tu wakiwemo walimu wameshaanza kulipwa. Wale ambao hawajalipwa naomba waendelee kusubiri, muda wao wa kulipwa ukifika watalipwa. Hakuna mtu yeyote ambaye hatalipwa deni ambalo ni halali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili ameuliza kwamba Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea allowance walimu? Napenda nimhakikishie kwamba Serikali ni mwajiri wa watumishi wote, siyo walimu peke yake. Kwa hiyo, kama ambavyo tumeweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba tunaweka kipaumbele cha kuwa na nyumba katika maeneo ambayo ni vigumu kupata nyumba kama maeneo ya vijijini ambako hakuna hata nyumba za kupanga kwa watumishi wote; watumishi wa afya, walimu na watumishi wengine, hivyo hivyo hatuwezi kubagua kwamba sababu ni walimu kwa sababu ni walimu, tuwaongezee allowance walimu peke yao watumishi wengine tuwaache gizani, hapana. Nadhani huo utakuwa ni ubaguzi na Serikali haiwezi kufanya hivyo.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Utakubaliana nami kwamba hakuna kada inayonyanyasika hapa nchini kama walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Serikali ilipunguza baadhi ya walimu wa sekondari kwenda shule za msingi kutokana na upungufu wa walimu na ikadai kwamba ina fedha za kuwalipa. Leo tunavyozungumza, baadhi ya Wakurugenzi wamewaambia wale walimu warudi kwenye shule za sekondari. Kwa hiyo, ina maana Serikali ilikuwa haijajipanga. Je, ni lini Serikali itawalipa walimu hao fedha kama ambavyo walidai kwamba watawalipa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Susan Lyimo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza uamuzi ule wa kuhamisha walimu wa sanaa waliozidi katika shule za sekondari kuwapeleka kwenye shule za msingi ulikuwa ni sahihi. Kilichosisitizwa ni kwamba mtumishi yeyote anastahili apate haki zake kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni zetu za Utumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tangazo la Mheshimiwa Rais limetoka mwezi Februari kwamba mtumishi asihamishwe mpaka alipwe, wale ambao walikuwa wameshahamishwa watalipwa madeni yao halali, wala hakuna tatizo. Wale ambao walikuwa bado, wasubiri, watahamishwa baada ya fedha kupatikana. Wale ambao wamerudishwa ni kwa muda tu. Kwa hiyo, naomba hili liwe clear wala halina matatizo yoyote.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika imejitahidi sana kuhamasisha wananchi kujenga vyumba vya madarasa na nyumba za walimu lakini bado kunahitajika nguvu ya Serikali kumalizia majengo yale ikiwemo Shule ya Msingi Busongola, Bulamata, Pandandogo na nyinginezo. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha hizo ili ziweze kumalizia majengo hayo ambayo wananchi wamejitolea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Moshi Selemani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa, kwa nchi nzima maeneo mengi kabisa wananchi wamejitahidi, wamejenga majengo na mengi ya majengo hayo yamefika kwenye lenta tayari kumaliziwa. Sasa hapo ni jukumu letu sisi Serikali, Halmashauri na wadau wengine kuunga mkono nguvu za wananchi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo tunalizingatia. Naomba sana tuwasiliane mwezi huu wa Julai na Agosti ili kusudi tuweze kuyatatua matatizo kama hayo.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali na pia kwa kukiri kwamba inaufanyia mapitio muundo na kwamba itazingatia mawazo ambayo nimeyatoa kutokana na swali langu, hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, wakati huu ambapo tunaelekea uchumi wa viwanda, ni matarajio kwamba Maafisa Biashara tulionao watakuwa na wajibu zaidi ya wajibu walionao sasa ambao kimsingi umejielekeza zaidi katika kufanya kazi ya kutoa leseni na kukagua leseni. Maafisa hawa wengi wao ni watu ambao wana elimu zao, wamesoma mambo ya international trade, international business na kadhalika, kwa hiyo, tunakuwa kama tuna wa- under utilize. Je, lini mipango hiyo ya kukamilisha muundo itakamilika? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali iko tayari wakati inaendelea kukamilisha suala hilo la muundo kuwa- task na kuwawezesha Maafisa Biashara ili waweze kuwasaidia wajasiriamali wetu kuibua miradi, kuwasaidia kuandika maandiko lakini pia kung’amua fursa mbalimbali za mikopo ya riba nafuu. Kwa mfano, kule kwetu Mafinga kuna wafanyabiashara na wajasiriamali wa mazao ya misitu kama mbao, mirunda na nguzo na majirani zangu Njombe wanalima maparachichi. Je, Serikali wakati inaendelea kukamilisha muundo huo iko tayari kuwa-task na kuwawezesha ili wafanye shughuli hizo za kuibua miradi? (Makofi). Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nirejee katika swali langu la msingi nimemshukuru sana kwa mchango wake. Hata haya maswali yake mawili ya nyongeza bado ameendelea kuweka mchango mzuri wa mawazo ambao utakuja kusaidia sana Serikali. Yeye ana uzoefu mkubwa, amefanya kazi katika Serikali za Mitaa sehemu nyingi sana, kwa hiyo, uzoefu wake tutautumia. Hata baada ya leo hapa namkaribisha ofisini kwangu ili tujadiliane kwa kina zaidi haya masuala ya Serikali za Mitaa kwa sababu wote tuna uzoefu nayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wajibu wa Maafisa Biashara, muundo utakapokamilika wataongezewa wajibu zaidi, kwa sababu sasa kama tunawatoa kwenye ile Idara ya Fedha tunawapeleka kwenye Idara nyingine ambavyo sipendi kuitaja kwa sababu haijawa rasmi watashirikiana huko na Maafisa Maendeleo ya Jamii na Wachumi katika kutekeleza yale ambayo Mheshimiwa Mbunge anayependekeza.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Kutokana na mwamko uliopo wa wananchi kujiunga na vikundi vya ujasiriamali pamoja na VICOBA lakini wananchi wamekabiliwa na kutokuwa na uwezo wa uzalishaji. Tatizo hili linachangiwa na kutokuwepo na Maafisa Biashara wa kutosha katika Halmashauri zetu na kuwajengea uwezo wananchi. Halmashauri zote nchini zina Afisa Biashara mmoja au wawili au hakuna kabisa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwaajiri Maafisa Biashara wa kutosha? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama alivyosema katika mazingira ya sasa kuna vikundi vingi vya uzalishaji mali, kuna VICOBA na shughuli nyingi za kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kutokana na kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Dkt. Kalemani na timu yake kueneza umeme vijijini na kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Profesa Mbarawa na timu yake kujenga barabara na sisi kupitia TARURA kujenga barabara za vijijini, fursa nyingi sana zinajitokeza. Kwa hiyo, kuna kazi kubwa sana iliyoko mbele yetu ambayo tunahitaji kuifanya kupitia kada hizi za Afisa Biashara, Maafisa Maendeleo ya Jamii na Wachumi. Serikali itahakikisha kwamba wanapatikana wa kutosha ili kusudi wananchi wahudumiwe vizuri. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa ukataji wa leseni unaenda sambamba na uwasilishaji wa tax clearence katika Halmashauri zetu na uwasilishaji wa tax clearance unaamaanisha kwamba watu wamelipa kodi, kwa maana hiyo watu wanalazimika kulipa kodi kabla hata ya kufanya biashara. Je, hatuoni kwamba ni muhimu kuondoa kigezo cha tax clearance katika baadhi ya biashara ili watu waweze kukata leseni na kuanza biashara kabla ya kulipa kodi na kabla ya biashara zenyewe kuanza? (Makofi) Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake linalenga kujaribu kutetea wafanyabiashara wale wanaoanza na utetezi wa aina hiyo siyo mbaya, ni mzuri. Hata hivyo, kwa sababu kuna kanuni, sheria na taratibu ambazo zimewekwa, nalichukulia swali lake kama mchango wa maoni ambao unahitaji kufanyiwa kazi baadaye lakini kwa leo hatuwezi kutoa tamko kwamba sasa tunafuta taratibu hizo. Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi hii ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa jitihada za kutoa mitaji kwa vijana na wanawake inabidi ziende sambamba na kuwajengea uwezo wa kuanzisha na kuendeleza biashara. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwatumia hawa Maafisa Biashara katika kuwajengea uwezo vijana wanaokuwa katika vikundi ambao wananufaika na asilimia 10 inayotengwa kutoka kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri? Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kwa dhati kabisa nimshukuru na kumsifu sana Mheshimiwa Zainab Katimba kwa sababu yeye amekuwa anashughulikia sana sana maslahi ya vijana katika Bunge hili Tukufu. Aliwahi kuleta mpaka mapendekezo ya hoja kutaka kutetea vijana wanaomaliza shule ili kusudi waajiriwe bila kuwa na experience. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimhakikishie kwamba vijana katika nchi hii wana idara nyingi sana za kuweza kuwasaidia mawazo ya kujikwamua kutoka pale walipo kwenda mbele. Katika Halmashauri kuna Idara ya Vijana, Idara ya Maendeleo ya Jamii na Idara ya Mipango sasa Maafisa Biashara tunawongezea sehemu nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana nitumie nafasi hii kuwaomba vijana wa nchi hii ambao hata fursa ambayo ziko katika Halmashauri hawazitumii ipasavyo, ukienda katika Halmashauri unakuta maombi ya vijana yako asilimia 10 ya maombi yote yaliyowasilishwa. Kwa kweli, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tujitahidi kuwaelimisha na kuwaomba vijana wajitokeze na wajiunge katika vikundi na watumie fursa zilizopo kwa ajili ya kujiendeleza na Serikali tuko macho katika kuangalia suala hilo linatekelezwa vizuri. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. RHODA E. KUNCHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na Serikali kuendelea kutenga maeneo ya kibiashara kwa ajili ya wajasiriamali wadogo, lakini bado kumekuwa na changamoto kubwa kwa wajasiriamali hawa wadogo hususani katika Manispaa ya Mpanda Mjini kwamba wamepelekwa kwenye maeneo ambayo miundombinu ya kibiashara pamoja masoko imekuwa na changamoto kubwa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia wajasiriamali hawa katika Manispaa ya Mpanda Mjini? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka juzi Serikali imetoa maelekezo kila Halmashari, Wilaya na mkoa kutenga maeneo maalum kwa ajili ya uwekezaji. Uwekezaji ni kuanzia uwekezaji mdogo, wa kati na mkubwa hususani maeneo ya viwanda, viwanda vidogo, viwanda vya kati na vikubwa na yawepo maeneo maalum kwa ajili ya biashara katika kila mji na kila Halmashauri. Kwa hiyo, hayo ni maelekezo ambayo yanakwenda kuboresha maeneo yetu ya Miji, Halmashauri na minada.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hayo maelekezo ya Serikali yatakapokamilika kutekelezwa vizuri, miundombinu ni sehemu ya mahitaji kwenye maeneo hayo mapya. Kwa hiyo, tunazidi kusisitiza kila halmashauri inapotenga eneo jipya lazima liambatane na miundombinu inayohitajika, ikiwemo umeme, maji na vyoo. Kwa hiyo, masuala yote ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyazungumza, kama ni Mpanda basi tutafuatilia tuhakikishe kwamba hiyo miundombinu inayokosekana inakuwepo. Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, Mheshimiwa Waziri amesema fedha za TARURA ni kidogo na yeye amepita barabara za Mbulu, hasa Tumati kwenda Martado ni mbaya sana. Je, atatusaidiaje kwenye kipindi hiki ili barabara zile ziweze kutengenezwa na wananchi wakaondoa ile adha ya kupita kwenye barabara ambayo haipitiki kwa sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyoeleza katika jibu la msingi na kama ambavyo amejibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa muuliza swali la msingi, Mheshimiwa Kwandikwa Naibu Waziri wa Ujenzi; taarifa ya tathmini ile ya kina ambayo tutaipata kuanzia kesho, hiyo ndiyo itakayotupatia taarifa sahihi ya barabara zote ikiwemo barabara ile ya kwenda Tumati ambayo tulipita na Mheshimiwa Mbunge kuanzia Yaeda Chini mpaka Tumati kule barabara si nzuri sana. Kwa hiyo, tutaiwekea utaratibu mzuri sana wa kipaumbele baada ya kuwa tumekubaliana vizuri zaidi na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi.
MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tatizo la barabara katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu linafanana kabisa na tatizo la barabara katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlowo katika Jimbo la Mbozi. Naomba kuuliza, ni lini sasa Serikali itatengeneza barabara ambazo zipo katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlowo, Jimbo la Mbozi, ambazo wakati wa mvua mara nyingi zimekuwa hazipitiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli. Tatizo alilolisema Mheshimiwa Mbunge katika eneo lake ni tatizo ambalo limekuwa likiikabili nchi nzima wakati wa masika wakati mvua kubwa zikinyesha, hasa barabara zetu ambazo huwa zinaathirika sana ni barabara za udongo na barabara za changarawe, ukiacha barabara za lami ambazo maeneo machache, hasa ya madaraja ndio huwa yanaathirika zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nimpe ndugu yangu comfort kwamba, suala hilo linatambulika Serikalini. Katika tathmini ambayo tunaifanya tumezingatia hilo ili tuwe na backup ya kutosha wakati wa mvua kuweza kukabiliana na changamoto ambazo huwa zinajitokeza wakati wa masika.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa, wananchi wa Yulansoni, Lelembo hadi Kitumbili ni wazalishaji wakubwa na barabara hiyo haimo kabisa kwenye mtandao na TARURA haiwezi kutengeneza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI alishatembelea huko na kutoa ahadi ya kutafuta pesa ili barabara hiyo itengenezwe. Je, ni lini barabara hiyo itatengenezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kiula, Mbunge wa Iramba Mashariki ambako tunaita maarufu Mkalama, lakini wenyewe tu hawajaleta ombi la kubadilisha jina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba, kuna changamoto kubwa sana katika eneo hilo lote la Mkalama. Wiki mbili zijazo nitatembelea Mkalama, tutapita mpaka hiyo barabara anayoitaja. Hata hivyo kwa hali halisi nitoe tu comfort kwa Bunge lako Tukufu na Wabunge wote, kwamba wenzetu Wahandisi, taaluma yao ni ya kuaminika kwa sababu wanajenga vitu vya kuonekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa si kwamba tunadharau taaluma nyingine, ila ni kwa sababu wanajenga vitu ambavyo vinaonekana. Kwa hiyo ili kusudi wafanye kazi zao vizuri, mazingira ambayo tunayaandaa kupitia tathmini ambayo tumeifanya ni kuhakikisha kwamba, tunaweka mazingira mazuri ili kazi zao watakazozifanya ziweze kuonekana vizuri zaidi kwa wananchi.
MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa Chombo cha TARURA ni kipya na kilipoandaliwa kilipewa fedha ndogo; na kwa kuwa fedha iliyotengwa na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo, anazifahamu sana barabara za Mpwapwa, barabara za mjini na barabara za Mima; je, TARURA iko tayari kuongezwa fedha ili zile barabara za Mpwapwa Mjini na Mima ziweze kutengenezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, kwanza katika sehemu ya kwanza ya swali lake, maana kauliza kama maswali mawili; ni kwamba TARURA iko tayari kuongezwa fedha, hiyo, niseme wazi. Pia jambo la msingi la pili ni kwamba tunajua mazingira yote katika Tarafa ya Mpwapwa na Tarafa ya Mima kwa sababu, aliuliza swali la msingi hapa na katika swali la msingi tukamuahidi kwamba, tutatuma wataalam. Wataalam wamekwenda kule wakiwemo Wahandisi walioko kwenye jimbo lake, wamefanya tathmini na wametuletea ofisini, hivyo, tutaifanyia kazi katika mwaka ujao wa fedha.
MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nichukue nafasi hii kushukuru kwa jibu zuri, fupi, linaloeleweka la Mheshimiwa Naibu Waziri. Hata hivyo, kwa maana ya uelewa wa pamoja nimwombe Mheshimiwa Naibu Waziri tuondoke pamoja twende tukatembelee hii barabara kutoka Zajilwa – Gongolo – Umoja hadi Izava, lakini pia na barabara kutoka Zajilwa hadi Itiso tuone, tushauriane tuone jinsi barabara ilivyo. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba, ombi alilotoa Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga tutalitekeleza.
MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Ni azma ya Serikali kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa na Wilaya mbalimbali. Mkoa wetu wa Manyara ambao una Makao Makuu Babati hakuna barabara ya lami inayounganisha Wilaya za Kiteto na Simanjiro na nyakati zingine hazipitiki kutokana na hali mbaya ya barabara hizo kuwa za vumbi na kwa kuwa iko kwenye Ilani kwa muda mrefu. Je, ni lini Serikali sasa itaunganisha barabara kutoka Simanjiro na Kibaya kuja Babati kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nilihakikishie Bunge Tukufu kwamba utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi unaendelea ambayo imeelekeza ujenzi wa barabara hizo kwa kiwango cha lami; na hasa hasa nikitaja barabara ambayo inatoka Kilindi inapita Kiteto inakuja mpaka Dodoma huku Kondoa ambayo ni barabara kumbwa sana itaanza kutengenezwa hivi karibuni chini ya usimamizi wa Wizara ya Ujenzi. Hii barabara ya kutoka Babati kwenda mpaka Simanjiro na ile aliyoitaja nyingine tunaziangalia kwa karibu sana na ndiyo maana matengenezo yake huwa ni ya uangalizi wa juu kabisa chini ya usimamizi ya Mkuu wa Mkoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wake umepelekea barabara hizo kuimarika na kwa sasa zinapitika muda wote wa mwaka isipokuwa matengenezo madogo madogo kama kuna mvua kubwa sana. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba utekelezaji utafanyika, naomba tu wananchi wawe na subira.
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Barabara zote zilizozunguka Mlima Hanang kutokana na mvua kutoka Gendabi, Hatgabadau, Katesh, Gitting, Gerodom na Gendabi zote zimeharibika. Naamini kwamba zitakuwa zimeoneshwa kwenye needs assessment. Je, Mheshimiwa Waziri anasemaje kwa sababu kuna makorongo makubwa yanayozuia akinamama kwenda hospitali na watoto kwenda shuleni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira ya Mikoa hii ya Manyara na Arusha yanafahamika, hasa maji yanapoporomoka kutoka kwenye milima yana tabia ya kuharibu barabara kwa haraka sana. Kwa hali hiyo, kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wangu amewaagiza Mameneja wa TARURA wote kufanya tathmini ya kina ili maeneo yale yaweze kupata uhakikisho maalum wa matengenezo ambayo yatahakikisha kwamba hayo maji hayaharibu kwa haraka barabara zetu katika maeneo hayo kama ambavyo imekuwa ikitokea. Napenda kumwahidi Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu kwamba tutalifuatilia utekelezaji wa agizo hilo kikamilifu ili maeneo hayo ili tuweze kuyapa kipaumbele kinachotakiwa. (Makofi)
MHE. SUSAN A. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Barabara ya Kimara - Bahama Mama - Msewe kwenda Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ilijengwa ili kuondoa msongamano katika Barabara ya Morogoro. Sasa magari haya yanapita Chuo Kikuu na Chuo Kikuu barabara imeharibika sana. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ile ya Chuo Kikuu kutoka Msewe kuelekea jengo la Utawala ili kufanya mandhari ya Chuo Kikuu iwe nzuri kwa sababu kwa kweli barabara hiyo imeharibu sana barabara za Chuo Kikuu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara aliyoitaja ni muhimu sana katika kupunguza msongamano wa magari katika Barabara ya Morogoro hasa kwa watu wanaokwenda maeneo ya City Centre. Hata hivyo, barabara ile ina changamoto ya ufinyu wake. Kama inatakiwa kutengenezwa vizuri basi inatakiwa fidia kubwa sana ilipwe kwa wananchi ambao wamejenga mpaka karibu na barabara, hasa kuanzia Kimara kuja kupita maeneo ya milima ya Golani, kuja kuteremsha chini kwenye daraja hapo kuna uvamizi mkubwa sana ambao ulifanywa na wananchi, barabara ile ni finyu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo matengenezo yake yanahitaji tathimini ya kina ambayo itaishauri Serikali namna ya kuiendeleza hiyo barabara. Naomba sana kwa sasa hivi matengenezo madogo madogo ambayo yanafanyika wananchi watuvumilie yaendelee hiyo hivyo mpaka ambapo tathmini ya kina itakapokamilika.
MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wakati fulani hili Bunge haya majibu tunayopewa tuwe tunayachunguza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 12 ambayo wameisema hapa, ni kweli kulitokea vurugu na mimi kama kiongozi, Mbunge nilipiga simu saa 12.00 asubuhi kwa Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kuwataarifu kwamba kuna vijiji viwili vinagombania ardhi na kuna watu wameenda kulima, akina mama wawili wakanyang’anywa ng’ombe kwa upande wa pili, tulivyokuwa tumepewa taarifa hizo. Saa 12.00 asubuhi viongozi wote wa Mkoa na Wilaya wakasema wamepokea taarifa, Jeshi la Polisi limekwenda pale saa 11.00 jioni watu wamepigana mpaka wameuana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi msako uliofanyika saa 11.00 jioni, tarehe 13 tulienda pale viongozi wote, Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa na vyombo vya habari vilikuwepo, maduka yote yamechukuliwa. Mambo mengine kusema hapa ni aibu, nachokiomba Serikali katika hili …
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu Serikali katika hili waende wakaangalie hiyo halisi ilivyokuwa na sisi tuna ushahidi wa kutosha juu ya jambo hilo. Hilo swali la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa chanzo cha mgogoro huo ni mgogoro wa ardhi ambao una vijiji vitatu ambapo kimsingi mgogoro ule ni kama umeisha. Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa aliyekuwepo Mheshimiwa Simbachawene alishafika pale akatoa maamuzi, maeneo yale yamegawanywa na vigingi vimewekwa. Ni lini sasa, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa itaenda kuweka GN kwenye maeneo hayo ili kumaliza mgogoro huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba uniruhusu nimsifu sana Mheshimiwa Boniphance Mwita Getere. Eneo analoliongoza lina changamoto nyingi sana hususani hizi za kiulinzi na kiusalama. (Makofi)
Mheshimiwa Mweyekiti, ombi lake aliloliomba, kwa sababu uchunguzi wa kipolisi bado unaendelea, haujakamilishwa kabisa, napenda nimhakikishie kwamba uchunguzi ule utaendelea kufanyika kwa kufuata taratibu za sheria za Polisi na sisi kupitia Kamati zetu za Ulinzi na Usalama, Mkoa na Wilaya tutafanya tathmini ya kina kuangalia matatizo gani yalijitokeza ili tuweze kuyatatua tukishirikiana naye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili, uwekaji wa GN kuondoa migogoro iliyokuwepo kwenye vijiji husika, naomba sana Mheshimiwa Mbunge awe na subira, suala hili linafanyiwa kazi kwa ujumla kwa nchi nzima. Tulikuwa na migogoro zaidi ya 366 katika nchi nzima na tunaifanyia kazi kwa pamoja. Kwa hiyo, kuweka usuluhisho wa aina hiyo kwenye eneo moja tu la nchi, tunaomba sana Mheshimiwa Mbunge awe na subira tunalifanyia kazi kwa nchi nzima. Ahsante sana.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Wabunge na Madiwani ni wawakilishi wa wananchi lakini mara nyingi baadhi ya Wabunge na Madiwani wamekuwa wakitoa taarifa za migogoro kati ya wananchi kwenye maeneo yao lakini matokeo yake ile migogoro inageuzwa Wabunge au Madiwani wanaonekana ni wachochezi wanakamatwa na kuwekwa ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niulize Serikali, ni lini tabia hii itakoma Waheshimiwa Wabunge na Madiwani wanapotoa taarifa ionekana kwamba taarifa hizo ni taarifa muhimu na za kufanyiwa kazi na ziheshimike? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Selasini, Mbunge wa Rombo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Vitongoji na Mitaa ni viongozi wa umma. Wanapotoa taarifa huwa zinapewa uzito unaostahili, isipokuwa tu kama kuna taarifa zingine ambazo zinakuja ku-counter kwamba labda wao wamehusika kwa njia moja au nyingine katika kusababisha mitafaruku iliyojitokeza hapo ndiyo hatua nyingine huwa inachukuliwa. Hata hivyo, taarifa zao huwa zinachukuliwa kwa uzito unaostahili na kwa heshima kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sema tu kwamba wenzetu wa Jeshi la Polisi kupitia Sheria ya Kanuni ya Adhabu wanao uwezo wa kufanya counter intelligence research kujua kwa kina tatizo hasa ni nini. Sasa wanaweza wakamshikilia kiongozi kwa muda ili waweze kupata taarifa za ziada, lakini kwa kweli kama watazidisha muda ambao wanaruhusiwa kukaa na viongozi kwa ajili ya mashauriano hiyo itakuwa wanafanya kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, swali lake ni la msingi na kwa kweli tutaliangalia kwa umakini zaidi ili kusudi kuweza kuweka mazingira mazuri zaidi. Sheria ya Kumlinda Mtoa Taarifa ipo na ilipitishwa na Bunge lako Tukufu. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi wowote.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Kakunda, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, je, atakuwa tayari kufika katika Wilaya ya Same ili kwenda kuona hali ambayo ipo sasa hivi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Wilaya ya Kilolo inajenga hospitali kubwa na nzuri, je, ni kiasi gani cha wahudumu au Madaktari wanaweza kuwatengea kwa msimu huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mwamoto na Mheshimiwa Dkt. Mathayo huko aliko kwamba nitafika Same baada tu ya Bunge la bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mwamoto kwa kufanya ufuatiliaji wa kina na wa karibu, katika kipindi cha miezi minne au mitano ameweza kufanikiwa na Serikali imepeleka pale zaidi ya shilingi bilioni nne kwa ajili ya kujenga hiyo hospitali ya wilaya na Mheshimiwa Rais juzi ameweka jiwe la msingi. Nimhakikishie tu kwamba tutashirikiana na wenzetu wa utumishi kuhakikisha hospitali ile inapata watumishi wa afya kwa mujibu wa kitange na uwezo wa Serikali.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii. Kwa kweli wananchi wa Wilaya ya Same kwa ujumla wao wanajitahidi sana kujenga zahanati. Ningemwomba Mheshimiwa Waziri aone umuhimu wa Serikali kwenda kuona jitihada zile, naomba atuambie hapa ndani atakwenda lini na atatoa msaada gani kwa sababu hali ya wananchi hasa wa milimani upande wa afya ni mbaya sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Anne Kilango Malecela na wananchi wote wa Wilaya ya Same kwamba nitakapokwenda katika Wilaya ya Same sitaishia katika Jimbo la Same Magharibi peke yake bali nitapita mpaka kwenye Jimbo la Same Msahariki. (Makofi)
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Nini utaratibu wa Serikali katika kuhakikisha wananchi au mashirika mbalimbali wakishajenga zahanati hizi kwa mfano Jimbo la Vunjo Zahanati ya Kochakindo ina zaidi ya miaka mitano ilijengwa na TASAF haina watumishi wala vifaa kwa ajili ya kutoa tiba. Utaratibu wa Serikali ni upi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu kwamba swali la Mheshimiwa James Mbatia linaonekana ni maalum kwa eneo maalum. Kwa hiyo, namwomba sana baada ya kikao hiki leo hii tuweze kuonana ili anipe details.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hata sisi viongozi wa Bunge mojawapo ya sifa ni kuwa na kazi halali zinazotuingizia kipato kama hawa Wenyeviti wa Vitongoji ambao sisi tunalipwa, wao hawalipwi. Je, Serikali iko tayari kuleta sheria ili waweze kulipwa mishahara? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa viongozi hawa ndiyo wanaohamasisha maendeleo kama ujenzi wa zahanati, shule za msingi, sensa na kusimamia amani, je, Serikali iko tayari iko tayari kuendelea kuwalipa posho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza, napenda nimhakikishie kwamba wakati wowote Serikali inapopata mapendekezo huwa inayafanyia kazi. Kwa hiyo, mara tutakapopata mapendekezo kutoka kwenye vikao halali vinavyohusika tunaweza wakati wowote tukafanya marekebisho ya sheria kutokana na muktadha wa muda utakavyokuwa na mapendekezo yatakavyokuwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu kulipa posho, Serikali ilishatoa Mwongozo tangu mwaka 2003 kwamba yatumike mapato ya ndani kulipa posho kwa viongozi hawa na posho zile zimeainishwa. Kwa hiyo, ni jukumu la Wakurugenzi wa Halmashauri na Mheshimiwa Mbunge namwomba sana asimamie kwenye jimbo lake na watumie Mwongozo huo kuhakikisha kwamba viongozi wetu hawa wanalipwa posho.
MHE. HASNA S. K. MWILIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Natambua kwamba Jimbo la Kigoma Kusini linakidhi vigezo vyote vya kugawanywa na kuwa majimbo mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu kwa mfano, Mkoa wa Katavi una kilometa za mraba 45,000 population 564,000. Jimbo hili la Kigoma Kusini lina vigezo vyote na tayari tulishafanya vikao kuanzia kwenye Vijiji, Kata, Baraza la Madiwani, DCC, vikao vikaenda mpaka kikao cha Mkoa kwa maana ya RCC na tayari tulipeleka Wizara ya TAMISEMI. Tume ya Uchaguzi mwaka 2015 waliliweka kwenye website yao kuonesha kwamba wako tayari sasa kuligawa, kama taratibu zote zilishafanyika na tulishawasilisha kwenye Wizara ya TAMISEMI, kwa nini walipotangaza majimbo mengine 2015 hawakuligawa jimbo hili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nguruka ilishafuata taratibu zote za kisheria na vigezo vyote inavyo kwa maana tuna kata nne na vigezo vya kisheria vinasema lazima tuwe na kata tatu. Je, kwa nini sasa Wizara ya TAMISEMI wasiamue tu rasmi kutangaza kwamba Mamlaka ya Mji wa Ngaruka sasa tayari inaweza kuanzishwa rasmi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza, nina wasiwasi aliposema kwamba ana uhakika Jimbo la Kigoma Kusini limekidhi vigezo vyote, lakini nilipokuwa najibu swali la msingi nilizungumza kigezo kimojawapo ni ukubwa wa ukumbi wa Bunge. Sasa sijaelewa kama kigezo hicho nacho tayari kimefikiwa kwa kuangalia ukubwa na viti vilivyomo ndani ya Bunge kama kweli vinaweza vikakidhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nimhakikishie tu kwamba kwa mawasiliano zaidi na kuwapa uhakika wananchi wa Kigoma Kusini tutapeleka barua Tume ya Taifa Uchaguzi ili kusudi watupe mrejesho mzuri zaidi wa hatua ambayo imefikiwa mpaka sasa hivi. Nina uhakika 2020 bado iko mbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu Nguruka kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo, naomba sana arejee jibu langu la msingi nimesema kwamba vikao vinatakiwa vianzie kwenye Serikali ya Kijiji, Halmashauri ya Kijiji ikae ipeleke kwenye Mkutano Mkuu wa Kijiji upitishe, upeleke kwenye Kamati ya Maendeleo ya Kata iende kwenye Halmashauri, iende Mkoani ndio ije kwetu kwa ajili ya kumshauri Waziri mwenye dhamana na Waziri mwenye dhamana ni Rais. Kwa hiyo, itakapofika kwetu tutatoa ushauri, naomba sana awe na subira.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Wilaya ya Tunduru ni miongoni mwa wilaya kubwa ina kilometa za mraba 18,786 sawa na Mkoa wa Mtwara wenye wilaya sita. Je, Serikali haioni wakati sasa umefika wa kugawa wilaya hiyo kulingana na majimbo yaliyopo, kuna Jimbo la Tunduru Kusini na Jimbo la Tunduru Kaskazini maeneo hayo sasa yakapata wilaya? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpe taarifa tu kwamba Jimbo la Sikonge ambako mimi natoka lina kilometa za mraba 27,873 sasa yeye kilometa za mraba 18,786 anaweza akasubiri sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwape comfort wananchi wa Tunduru kwamba maeneo haya Serikali inafahamu kwamba ni makubwa, lakini kwa sasa hivi mzigo uliopo kwa Serikali ni kuhakikisha kwamba inaziwezesha wilaya mpya ambazo zimeanzishwa hivi karibuni, tuna wilaya kama sita ambazo zimeanzishwa hivi karibuni zipate majengo, vifaa vya uendeshaji, zipate watumishi, huo mzigo bado ni mkubwa sana na halmashauri mpya vilevile. Kwa hiyo, tukimaliza kuziwezesha hizi halmashauri mpya na wilaya mpya zikapata vifaa na majengo yakakamilika kabisa hapo ndiyo tutakuja kwa awamu nyingine sasa ya kuanzisha wilaya mpya na halmashauri mpya.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Wananchi wa Kata za Isaka, Mwalugulu, Isakajana pamoja na Mwakata walishakamilisha mchakato wa kuanzisha Halmashauri au Mamlaka ya Mji Mdogo wa Isaka na taratibu zote ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri amezielezea hata hapa hadi kufika hatua ya kufika kwenye ofisi ya Waziri mhusika wameshafikia. Nataka kujua tu ni lini sasa hatimaye Mamlaka ya Mji Mdogo wa Isaka itaanzishwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Ezekiel Maige kwamba maombi ya Mamlaka ya Mji Mdogo wa Isaka yameshapokelewa, yanafanyiwa kazi, lakini tunawaomba wananchi wasubiri pale ambapo tutakuwa tayari mara moja tutatangaza.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Manispaa ya Moshi Mjini tayari imekidhi vigezo vyote na kikubwa zaidi ina Mlima Kilimanjaro ambayo ni highest pick in Africa. Nataka kujua process inaendelea vipi mpaka sasa hivi bado hatujapata majibu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, sijamwelewa vizuri Mheshimiwa Susan Lyimo kwa sababu Moshi tayari ni Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, okay kuipandisha kuwa jiji. Pamoja na alivyosema kwamba imekidhi vigezo lakini bado hatujapata maombi rasmi kutoka kwenye vikao vinavyohusika kwa hivi karibuni….
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kama anazungumzia maombi ya zamani lakini ya hivi karibuni hatujapata.
MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nachelea kusema level ya seriousness kwenye hili jambo bado ipo chini sana. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2016/2019 Serikali ilitenga shilingi milioni 750 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni katika shule za sekondari kwenye kata zenye mazingira magumu, lakini kwenye taarifa hii ya utekelezaji ukurasa wa 132 mpango huu umetekelezwa kwa asilimia sita tu. Ningependa kufahamu, ukiwa umebaki mwaka mmoja kukamilika kwa mpango huu ni lini sasa Serikali itakamilisha ujenzi wa wabweni haya kwenye shule kumi ili kupunguza adha kwa wanafunzi wa kike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Serengeti yenye Kata 30 ina shule za sekondari kwenye Kata 21 tu na Kata 9 hazina shule za Kata. Kata hizo ni Lung’avule, Getasamo, Kiambai, Morotonga, Sedeko na kadhalika. Ningependa kufahamu ni lini sasa Serikali itakamilisha ujenzi wa shule za sekondari kwenye hizi kata tisa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ruge amenukuu Mpango wa Taifa wa miaka mitano na mimi kwa niaba ya Serikali napenda nimuhakikishie kwamba mpango ule tunaendelea kuutekeleza mwaka hadi mwaka na itakavyofika mwisho mwaka wa utekelezaji wa mpango wa miaka mitano, malengo mengi yaliyomo yatakuwa yametekelezwa. Mheshimiwa Mbunge naomba asiwe na wasiwasi na awaarifu wananchi ambao anawawakilisha kwamba tutatekeleza mpango ule na utakapofika mwisho wa mwaka utekelezaji wake tutakuwa tumefikia malengo mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameuliza kwenye Wilaya ya Serengeti kwamba ina kata 30; kata 21 zina shule za sekondari na kata tisa hazina shule za sekondari na akauliza lini tutajenga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali lake la msingi ni wazi kwamba kata hizo ambazo hazina shule sekondari wanafunzi wake ni miongoni mwa wanafunzi ambao wanatembea umbali mrefu kufuata shule kwenye kata za jirani. Nimehimiza kwenye jibu la msingi kwamba Halmashauri iendelee kushirikiana na wadau wengine pamoja na wananchi kuhakikisha kwamba Kata hizo zinaanza ujenzi wa shule na Serikali itaingia kusaidia mara watakapoanza ujenzi huo. (Makofi)
MHE. JOYCE B. SOKOMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa Mkoa wa Mara ilionekana kwamba mtoto wa kike hana thamani kwa upande wa elimu. Sasa Serikali imeona kabisa kwamba kuna shida ya mabweni ya watoto wa kike. Mtoto wa kike anapotoka shule kwenda nyumbani anakwenda kufanya kazi za nyumbani na anapotoka tena nyumbani kwenda shuleni ni umbali mrefu anafika amechoka sana.
Kwa nini Serikali isichukue hatua ya haraka kuhakikisha inajenga mabweni katika shule za Mkoa wa Mara? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema ni kweli katika baadhi ya mazingira tunaweka kipaumbele kujenga mabweni kwa mfano katika maeneo ya wafugaji na baadhi ya maeneo katika baadhi ya mikoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya kujenga mabweni kwenye kila shule ya sekondari nchini ni kubwa sana, lakini vilevile katika mazingira ambayo shule imesajiliwa kama shule ya kutwa kwa mazingira yake siyo vizuri sana kuweka mabweni wakati mtoto anaweza akatembea umbali wa kilomita mbili, moja ama mita 500 akafika shuleni. Kwa hiyo, ni jambo ambalo tunaliangalia case by case kwa mazingira na tunahimiza kwamba wazazi, wananchi na Halmashauri zijenge dahania (hostel) ambazo zitasaidia hasa watoto wa kike wasitembee umbali mrefu kwenda nyumbani na shuleni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hicho ndicho kitu tunachohimiza na Serikali itawaunga mkono katika kuendesha yale mabweni. Shule ikipandisha hadhi tu ikapata hadhi ya kuchukua wanafunzi kutoka mikoa mingine, Serikali inaingiza mkono moja kwa moja hapo kusaidia, ahsante. (Makofi)
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niseme tu kwamba kwa kuwa Serikali imeonekana inapeleka pesa kidogo sana ya maendeleo kwenye sekta hii ya kilimo hasa katika jimbo langu na kwa hiyo Maafisa Ugani wanakuwa wanakosa kazi za kufanya. Je, Serikali haioni ni kupoteza hela za Serikali kama watazidi kuongeza waajiriwa wakati hawana kazi za kufanya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; ni wazi kwamba Maafisa Ugani hawa wanaopelekwa kwenye vijiji hawajawahi kufanyiwa semina, wengine wana miaka kumi, wala orientation ya kwamba kazi ambazo wanatakiwa wazifanye kwa kipindi hiki ni nini na kwa kuwa ukijua kwamba kozi wanazochukua haziko specific kwenye mazao yale, mtu ametoka kulima korosho leo anapelekwa kwenye ndizi, hajui hata kutengeneza migomba.
Je, Serikali haioni kwamba haijawatendea haki maafisa ugani hawa wanaopelekwa vijijini bila kufanyiwa semina na orientation za kuwafanya waelewe kile wanachotakiwa kufanya katika vijiji au kata zile pamoja na kwamba pia hawana vitendea kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza amesema kwamba Serikali inapeleka bajeti ndogo, nimwambie tu kwamba bajeti inayopelekwa na Serikali Kuu katika Halmashauri ni sehemu ndogo tu ya bajeti ya jumla ambayo Halmashauri inatakiwa ifanyie kazi. Maana yake kule kuna bajeti ya ndani inaitwa own source budget. Kwa hiyo hakuna sababu yoyote inayokubalika inayomfanya Afisa Ugani yeyote aseme kwamba ameshindwa kwenda kijijini eti kwa sababu ya bajeti ndogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili amesema kwamba kuna Maafisa Ugani wamepelekwa kule lakini hawana ujuzi na mazao husika. Sisi Serikali tunachokifanya tunapeleka Afisa Ugani ambaye amesomea Sekta ya Kilimo, Sekta ya Mifugo kwenda kufanya kazi za ugani katika Halmashauri fulani, sasa akikuta kule kuna zao fulani mahususi ni kazi yake kujiridhisha kupitia tena, kudurusu documents mbalimbali zinazohusu zao hilo mahususi ili awe vizuri kitaaluma na kiuendeshaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nakubaliana naye kwamba mtu ambaye amesoma general agriculture akienda kwenye zao la tumbaku specific atalazimika kukosa baadhi ya utaalam katika zao lile, ni kweli, lakini tunawahimiza kwamba lazima wahakikishe kwamba wanalifahamu hilo zao vizuri na waweze kuwashauri wakulima vizuri kwa sababu wao ni wataalam wa kilimo. Kama mimi ni mchumi lakini nilisoma shule ya kilimo nakumbuka masomo ya kilimo wakati ule, je mtu ambaye amesoma cheti au diploma au ana degree ya kilimo, lazima atakuwa anajua vizuri zaidi. Ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. DKT. MARY M. MWANJELWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze pia na mimi kujibu swali la mama yangu, Mheshimiwa Kaboyoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri sana ya Naibu Waziri kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba na mimi niongezee hapo kidogo kwamba sisi kama Wizara ya Kilimo kupitia vyuo vyetu vyote vya mafunzo nchini, swali ambalo na mimi niliweza kulijibu jana, ni kwamba tumefanya mpango mkakati hata wale Maafisa Ugani ambao pia bado hawatoshelezi na tumesema wasikae ofisini, lakini tuna mpango mkakati kama Wizara ya Kilimo kuhakikisha kwamba tunawajengea uwezo hata wale ambao Maafisa Ugani wako maofisini ili waweze kutoa mafunzo kwa wakulima kuendana na mazao ambayo yapo katika hayo maeneo. Naomba kuwasilisha.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa matatizo ya ukosefu wa Maafisa Ugani inawakumba wananchi wa Jimbo la Ukonga katika Wilaya ya Ilala katika kata za Kitunda, Vigewe, Majowe na Mzinga. Wananchi wa eneo hilo ni wakulima wa mbogamboga na matunda lakini kuna Afisa Ugani mmoja anahudumia kata tatu, je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza Maafisa Ugani katika Jimbo la Ukonga na Wilaya ya Ilala kwa ujumla?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna upungufu wa Maafisa Ugani nchini, na kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba kwa maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi tunahitaji kuongeza Maafisa Ugani ambapo tukiwafikia hawa ambao tumepanga kuwaongeza kupitia maelekezo ya Ilani tunaamini tutakuwa na Maafisa Ugani wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali ina kibali cha kuajiri watumishi takribani 52,000 na mpaka sasa hivi hatujafikia hata 20,000 katika kuajiri, kibali ambacho kitatoka hivi karibuni labda mwezi wa pili au wa tatu, tutaajiri Maafisa Ugani wa kutosha kupunguza tatizo lililopo. Naamini tutakapoajiri hao kabla ya mwezi wa sita na kata hizo ambazo umezitaja tutazipatia Maafisa Ugani. Ahsante sana.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi tukizungumza Maafisa Ugani tunazungumza zaidi habari ya maafisa hawa wa kilimo, lakini kuna wanaohusika na uvuvi, kuna wanaohusika na ufugaji na ni dhahiri kwamba upungufu ni mkubwa.
Sasa swali langu ni hili, kuna maeneo kama Jimbo langu la Rombo vijana ambao wamesoma kwenye vyuo vya kilimo, vyuo vya uvuvi na vyuo vya ufugaji wanajitolea kusaidia wakulima au wastaafu wanajitolea kuwasaidia wakulima na wanatumika vizuri sana. Je, Serikali iko tayari kuwatambua hawa na kuwasaidia ili waendelee kuwasaidia wakulima wakati utaratibu wa kuongeza watumishi wengine ukiendelea kufanyika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, dhana ya kujitolea au volunteering kwa Tanzania na vijana wetu na wengine wastaafu, kwa wastaafu kidogo naona inatia matumaini lakini kwa vijana ambao wamemaliza vyuo bado haijaingia vizuri katika fikra zao.
Mimi nadhani katika nchi kama India huwezi kupata ajira kabla kwanza hujapata uzoefu kupitia hata kujitolea, kwa hiyo tunahamasisha sana pale ambapo wapo wataalam wetu ambao wanaweza wakajitolea kwenye kijiji, Halmashauri ifikirie namna ya kuwaratibu na kuwapatia posho kidogo ili waweze kufanya kazi zao vizuri sana. (Makofi)
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na nitahamasisha wadau kuvuta subira. Nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaendelea na mchakato wa kupata Halmashauri ya Mji wa Bagamoyo, je, ni lini Serikali itawaagiza Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo kuwalipa Wenyeviti wa Vitongoji malimbikizo yao ya posho ambayo hayajalipwa kwa mda mrefu sasa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa vile Bagamoyo siyo Halmashauri ya Mji kwa hiyo hatuna fursa ya mafungu makubwa ya ujenzi wa miundombinu ya barabara. Sasa naomba kujua ni nini kauli ya Waziri kuhusu kutusaidia Bagamoyo mafungu ambayo yatatuwezesha kujenga miundombinu ya barabara na mifereji ambayo iko katika hali mbaya sana katika Mji wa Bagamoyo na Vijiji vya Bagamoyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze na kumshukuru kwa kukubaliana na majibu kwenye swali la msingi na hili la kuwaomba wananchi wawe na subira wakati mchakato unaendelea, namshukuru sana kwa hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza amesema kwamba Wenyeviti wa Vitongoji hawajalipwa kwa muda mrefu na mimi napenda kumhimiza Mkurugenzi wa Halmashauri wa Wilaya ya Bagamoyo kutekeleza maagizo ya Serikali ambayo yanamtaka arejeshe asilimia 20 ya mapato yanayokusanywa kutoka kwenye kata husika ili yatumike, pamoja na kazi zingine, kulipa posho za Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji kwenye maeneo yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili amesema Mji wa Bagamoyo kweli una mahitaji ya miundombinu kama barabara na mifereji na amesema kwa usahihi kabisa kwamba itakapokuwa ni Halmashauri ya Mji ambayo inatakiwa iwe na sifa fulani kwa upande wa miundombinu sasa tuanze kupeleka mafungu kwa ajili ya kuanza ujenzi wa miundombinu hiyo. Mimi namuomba sana Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane hata baada ya Kikao hiki cha Bunge ili tuone ni namna gani mwakani tunaingiza kwenye bajeti ya TARURA huu ujenzi wa miundombinu ambao anaipendekeza.
MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Waziri. Pamoja na majibu yake mazuri nina maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza ni kuhusiana na uhalisia na Mto Ngarenanyuki. Mto huu ni moja ya mito michache ambayo imetokea katika maeneo yaliyohifadhiwa, unatokea katika Hifadhi ya Taifa ya Arusha, chanzo chake ni salama na unapitisha maji mengi ya kutosha na kutiririsha katika nyanda za chini ambapo unapotoka ndani ya hifadhi, kijiji cha kwanza unafikia Kijiji cha Ngarenanyuki yanatiririka mpaka Kijiji cha Ngabobo na zamani za kale yalikuwa yanatiririka mpaka Kijiji cha Jimbo langu la Longido cha Ngereani.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba; kwa kuwa maji haya yalipoingia Kijiji cha Ngarenanyuki wananchi wakagundua kwamba ni maji safi ya kuoteshea nyanya; wamekatakata mto mifereji mashine za kunyonya maji mtoni mpaka mto ukakaushwa na maji hayatiririki tena kwenda kwenye vile vijiji vya kusini zaidi. Serikali ina mpango gani wa kusanifu miundombinu ya umwangiliaji wa kisasa itakayowezesha matumizi bora ya maji haya ili yaendelee kutiririka kufikia jamii zilizo chini zaidi kwenye nyanda za chini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa tunakabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchi na uwezekano wa maji haya kutosha wakulima wa nyanya waliopo Ngarenanyuki, Ngabobo Mpaka Ngereani kuwafikia wote kwa mtiririko wa asili. Serikali haioni kwamba ni bora sasa wajenge tanki kubwa la kuvuta maji Ngereani ili nao waendeleze kilimo cha umwangiliaji wa nyanya; hasa ukizingatia kwamba ni kilomita 10 mpaka 20 tu katikati Ngereani kutoka mtoni?
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stephen Lemomo Kiruswa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yake yote mawili yamegusa utaalam ambao upo ndani ya Serikali ingawa haupo ndani ya Wizara yangu. Ni jambo la msingi alilolizungumza, kwamba kila Mtanzania anawiwa na dhima ya kulinda rasilimali za maji na hasa hasa kwa sababu haya maji mazuri yametoka katika eneo limeifadhiwa yalikuwa yanatiririka vizuri kwenda kwenye vijiji. Sasa wananchi wameya-tap na kuyachota na kupeleka kwenye miradi ya umwagiliaji bila kuzingatia ushauri mzuri wa kitaalam wa kutumia maji kidogo na kuzalisha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, basi natoa ushauri kwa Tume ya Umwagiliaji kwa kushirikiana na Mamlaka ya Bonde washirikiane, kwa sababu hizi ni mamlaka za Serikali, waende katika eneo husika wakawaelimishe wananchi kuhusu kilimo bora cha umwangiliaji bila kuchukua maji mengi kutoka kwenye mto ule ili maji yale yaifadhiwe yaendelee kutumika vile vile kwa shughuli zingine na kwa ajili ya vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kuhusu ujenzi wa tanki kubwa litatokana na ushauri ambao wataalam wataona kadri inayofaa katika kutumia maji ya Mto Ngarenanyuki. Ahsante sana.
MHE. SONIA J. MAGOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyogeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa wakulima wengi wa mihogo ni wadogowadogo na hawana mitaji na wamehamasishwa na wawekezaji kulima zao hili kwa wingi, je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wakulima hawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, vilevile napenda kujua Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia elimu wakulima hawa ili waweze kuzalisha zao hili kwa wingi na kwa kiwango kinachohitajika?
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sonia Magogo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kwamba wakulima wengi ni wadogo, hawana mitaji, kwa kweli hilo sio kwenye sekta ya kilimo cha muhogo peke yake bali wakulima wetu wengi hapa Tanzania hasa hawa wadogowadogo wanalima kilimo cha kawaida, kilimo cha kutegemea mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la muhimu zaidi ni pale alipouliza katika sehemu ya pili ya swali lake kuhusu elimu, hilo ndilo jambo la muhimu zaidi kwa sababu elimu itahusu kilimo bora cha muhogo, utafiti na kutumia mbegu bora. Kwa hiyo, tunashirikiana kwa karibu sana sisi mapacha, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda kuhakikisha kwamba mkulima anaongeza uzalishaji kutokana na ile elimu atakayopata kutoka kwa Maafisa Ugani walioko kwenye kata na vijiji. Hilo ndiyo jambo la msingi sana. Waziri wa Kilimo ameshaagiza Maafisa Kilimo wote nchini wale ambao hawajayajua vizuri mazao fulani kwenye maeneo yao wanatakiwa wapatiwe mafunzo wao wenyewe kwanza kabla hawajaenda kuwapatia wakulima. Ahsante sana.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada za Serikali kuona inainua kilimo hiki au zao hili la muhogo ambalo ni tegemeo kubwa hususan kwa watu wa Mikoa ya Kanda ya Mashariki, lakini zao la muhogo linakabiliwa na magojwa ya Cassava Mill Bags. Je, nini kauli ya Serikali kukabiliana na wadudu hawa ambao wanaathiri sana zao la muhogo ambalo linawarudisha nyuma wakulima wanaolima zao hili?
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Alichokisema ni kweli kabisa na haya masuala ya magonjwa ya mazao siyo kwamba yapo kwenye kilimo cha muhogo peke yake, bali mazao mengi yamekuwa yakiathiriwa sana na wadudu. Mheshimiwa Waziri wa Kilimo ameshatoa msisitizo na ametoa maagizo kwamba viuatilifu ambavyo ni feki visitumike kwenye mazao. Yeyote ambaye atakamatwa anauza au anampatia mkulima viuatilifu feki ambavyo havisaidii kupambana na magonjwa na wadudu atachukuliwa hatua kali na Serikali. Kwa hiyo, hiyo ni elimu mojawapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imechukua hatua za makusudi kabisa na kupitia vituo vya utafiti kikiwemo Kituo cha Utafiti cha Naliendele na kituo cha utafiti ambacho kipo chini ya Wizara ya Kilimo cha pale Dar es Salaam wamefanya utafiti mzuri wa mbegu ambayo inahimili magonjwa kama hayo. Kwa hiyo, msisitizo ni kutumia mbegu ambazo zinahimili matatizo hayo.
MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo walilonalo wananchi wa Tanga linafanana sana na tatizo walilonalo wananchi wa Mkoa wa Singida. Jimbo la Singida Kaskazini na Mkoa wa Singida kwa ujumla ni wakulima wakubwa sana wa vitunguu pamoja na alizeti. Hivi tunavyozungumza, soko la kitunguu gunia moja linauzwa kati ya shilingi 10,000/= mpaka shilingi 40,000/=, badala ya shilingi 80,000/= mpaka shilingi 120,000/= ilipokuwa katika msimu wa mwaka uliopita.

Je, Serikali iko tayari kuingilia kati suala hili na kuwanusuru wananchi ambao wanaendelea kupata hasara kutokana na kazi kubwa waliyofanya?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli alichokisema. Kwanza tunatoa tahadhari kwa Watanzania, wakulima pamoja na wafanyabiashara, lipo tatizo hapa nchini ambalo ni kubwa, watu wanakuja katika vijiji kununua, wengine wananunua kwenye mashamba bila kufuata utaratibu. Hilo tunashirikiana na Wizara ya Kilimo na tunashirikiana na Shirika la Vipimo kuhakikisha kwamba utaratibu wa kisheria unafuatwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hao watu ambao wamekuwa wananunua halafu wanasafirisha nje ya nchi bila kuwa na vifungashio vinavyokubalika kisheria, hao wanakiuka sheria na kwa kweli itabidi tuchukue hatua kali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuingilia kati suala la bei, namuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaingilia kati na tutatoa maagizo kwa maandishi kuanzia leo.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Hivi karibuni Mheshimiwa Rais alizindua mradi mkubwa sana wa maji kule Arumeru Magharibi, lakini wakati huohuo Arumeru Mashariki kuna shida kubwa ya maji kiasi kwamba wananchi wanaoga na kunywa maji ya shallow wells. Je, ni nini mkakati wa Serikali kutatua changamoto hii? (Makofi)
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, ni kwamba baada ya uzindizi wa mradi ule ambao ni mradi mkubwa sana wa maji katika Jiji la Arusha na viunga vyake likiwemo eneo la Arumeru Mashariki. Mikakati ya Serikali ni kutekeleza mradi huo ambao umeanza kutekelezwa mwaka huu wa fedha ambao utakamilika mwaka 2022 na vilevile kuweka mkazo kwenye uchimbaji wa visima virefu vya maji kwenye eneo la Uwanja wa Ndege na eneo la Magereza ambalo litatosheleza kabisa maji katika Jiji la Arusha na viunga vyake, likiwemo Jimbo la Arumeru Mashariki. Ahsante sana. (Makofi)