Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Joseph George Kakunda (23 total)

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Barabara ya Ipole - Mpanda yenye urefu wa kilometa 359 iliyoko kwenye mpango wa kujengwa kwa lami iko kwenye hali mbaya sana kutokana na kuharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha, maji maji yamejaa kuvuka barabara na maeneo mengine yanatitia kiasi kwamba mabasi ya abiria na magari ya mizigo yanapata shida kupita na wananchi wa Tabora, Sikonge na Katavi nao wanataabika sana na barabara hiyo.
(a) Je, Serikali inachukua hatua gani za dharura za muda mfupi kuwasaidia wananchi wa Tabora, Sikonge, Katavi na maeneo mengine wanaoathirika na tatizo hilo?
(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kufanya mapitio ya haraka ya usanifu wa barabara hiyo ili kunyanyua zaidi tuta na kuongeza madaraja na makalvati ili kudhibiti maji ya mvua yasiharibu barabara mpya itakayojengwa?
(c) Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa lami na kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye sehemu (a), (b) na (c), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mwezi Januari hadi Machi mwaka 2016 Mikoa ya Tabora na Katavi ilipata mvua nyingi na sehemu ya barabara ya Tabora, Ipole, Koga hadi Mpanda kuharibika, hususan Mto Koga kujaa maji na kupita juu ya daraja la Koga. Hali hii ilisababisha barabara ya Tabora - Mpanda, sehemu ya Ipole hadi Nyonga, kufungwa kwa muda Serikali ilichukua hatua za haraka za kuifanyia matengenezo ya dharura barabara hii baada ya mafuriko kupungua.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, barabara mbadala ya Tabora - Uvinza hadi Mpanda, ilipatiwa pia matengenezo ya dharura ili Mkoa wa Katavi usijifunge kabisa. Kwa kuwa maji yamepungua, hatua nyingine ambazo zimechukuliwa ni pamoja na kuruhusu magari madogo na mepesi kuanza kutumia barabara ya Tabora hadi Mpanda. Serikali itafanya mapitio ya usanifu wa kina, wakati wa utekelezaji wa ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Tabora hadi Mpanda. Ujenzi wa barabara hii unategemea kuanza katika mwaka wa fedha 2016/2017 chini ya ufadhili wa Serikali ya Tanzania na Benki ya Maendeleo ya Afrika.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Mradi wa REA unaendelea kutekelezwa katika vijiji 24 katika Jimbo la Sikonge lakini mradi huo ulisimamia kwa muda mrefu ambapo baadhi ya maeneo nguzo zilizoachwa barabarani zimeanza kufukiwa na mchanga kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha:-
(a) Je, Serikali itakamilisha lini mradi huo kwa Awamu ya Kwanza na Pili?
(b) Je, Awamu ya Tatu ya utekelezaji wa mradi huo itahusisha vijiji gani katika Wilaya ya Sikonge na ni lini utaanza na kukamilika?
(c) Je, Serikali haioni umuhimu wa kufikisha umeme wa REA kwenye mitambo ya kusukuma maji ya Ityatya, Uluwa, Makazi, Igumila, Majojolo na Kiyombo ili kupunguza gharama za dizeli ambazo zimekuwa zikiathiri upatikanaji wa maji kutokana na gharama kubwa za uendeshaji mitambo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Sikonge ilijumuishwa kwenye REA Awamu ya II ambayo inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016. Kazi ya kupeleka umeme Wilaya ya Sikonge inajumuisha pia ujenzi wa umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 166.44 lakini pia ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 58.06. Kazi hii pia itajumuisha ufungaji wa transfoma 28 za ukubwa mbalimbali pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,704.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huo ambao unatekelezwa kupitia mkandarasi CHICCO umekamilika kwa asilimia 88 hadi sasa. Ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 umekamilika kwa asilimia 86 na ujenzi wa msongo wa kilovoti 0.4 umekamilika kwa asilimia 89.3, lakini pia transfoma 15 zimeshafungwa na wateja 228 wameunganishiwa umeme. Kazi hii imegharimu shilingi bilioni 6.42.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini REA, Awamu ya III, unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2016. Mradi wa REA Awamu ya III unakusudia kupeleka umeme katika vijiji vyote vilivyobaki vya Mheshimiwa Mbunge pamoja na shule, zahanati na vituo vya afya. Kadhalika, kazi hii itajumuisha kupeleka umeme kwa wananchi wapatao 1,510. Kazi hii inagharimu pia jumla ya shilingi milioni 4.33.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye pampu za kusukuma maji alizozitaja Mheshimiwa Mbunge za Ityatya, Makazi na Uluwa itafanywa na REA Awamu ya III. Kazi ya kupeleka umeme kwa vijiji na pampu hizi itahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa tisa, lakini pia ufungaji wa transfoma tatu pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 141. Kazi hii itagharimu shilingi milioni 317.14. Aidha, pampu za maji za Igumumila, Kiyombo na Magolo zitafanyiwa tathmini kubaini mahitaji yake ili na zenyewe ziweze kupatiwa umeme haraka iwezekanavyo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Kati ya mwaka 1954 na 1957 kulifanyika zoezi la upimaji wa maeneo ya Hifadhi za Misitu, Mapori ya Akiba na Hifadhi katika Wilaya ya Sikonge ambapo kulikuwa na wakazi takribani 16,000 na ng’ombe wapatao 2500. Kwa sasa wakazi wameongezeka hadi kufikia takribani 300,000 na ng’ombe wapo takribani 200,000 lakini eneo la kuishi, kulima na malisho ya mifugo na shughuli nyingine za kiuchumi ni lile lile la asilimia 3.7 ya eneo lote la Wilaya huku eneo la Hifadhi likibaki asilimia 96.3 na hali hii inasababisha migogoro kati ya wakulima, wafugaji na warina asali dhidi ya Maafisa Maliasili.
(a) Je, ni lini Serikali itawaongezea wakazi wa Wilaya ya Sikonge eneo la kuisha, kulima na kulishia mifugo kutoka asilimia 3.7 hadi angalau asilimia 25 ya eneo lote la Wilaya?
(b) Je, Serikali haioni kuwa kuongeza eneo la Wilaya hiyo kwa asilimia 25 kutaepusha migogoro iliyopo sasa na hivyo wananchi watatekeleza shughuli zao kwa amani na utulivu huku wakilinda mazingira pamoja na hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye sehemu (a) na
(b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na takwimu za Taasisi ya Takwimu ya Taifa (The National Bureau of Statistics) na Sensa ya mwaka 2012, Wilaya ya Sikonge ina ukubwa wa kilometa za mraba 27,873 na idadi ya watu wapatao 179,883. Aidha, maeneo ya hifadhi za misitu na wanyamapori yana ukubwa kilometa za mraba 20,056.94 sawa na asilimia 72 ya eneo lote la Wilaya, hivyo kufanya eneo la makazi na shughuli nyingine za binadamu kuwa sawa na asilimia 28.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi za misitu na mapori ya akiba katika Wilaya ya Sikonge ni muhimu kwa uhifadhi na maendeleo ya sekta nyingine, ikiwa ni pamoja na kuwa vyanzo vya mto Ugalla, ziwa Sagara, Nyamagoma na ardhi oevu ya Malagarasi - Moyowosi. Kwa mantiki hiyo, kugawa maeneo haya na kuruhusu shughuli za kibinadamu kutahatarisha upatikanaji wa rasilimali za maji kwa ajili ya shughuli za uvuvi, kilimo, ufugaji, matumizi ya nyumbani na mengineyo kwa kiasi kikubwa. Muhimu zaidi ni mchango mkubwa wa misitu hiyo katika hali ya hewa na udhibiti wa mabadiliko hasi ya tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imethibitika kwamba kilimo cha kuhama hama, ikiwa ni pamoja na utumiaji wa maeneo makubwa ya ardhi; ufugaji wa kuhama hama ukijumuisha uingizaji wa mifugo katika maeneo yaliyohifadhiwa, ni matumizi mabaya ya rasilimali ardhi na yasiyo na tija kwa Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi nitumie nafasi hii kuwakumbusha na kuwaomba wananchi kwa kushirikiana na uongozi wa Halmashauri za Wilaya husika, kuchukua hatua za makusudi kuandaa na kutekeleza mipango ya matumizi bora ya ardhi; hatua ambazo zitasaidia kuondoa changamoto za mahitaji ya ardhi katika Wilaya zote nchini ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Sikonge iliyoko Mkoani Tabora.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itakiboresha Chuo cha Maendeleo ya Jamii yaani FDC Sikonge ili kilingane na Vyuo vya VETA kwa kuogeza idadi ya walimu na mafunzo yanayotolewa?
NAIBU WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya vyuo 55 vya Maendeleo ya Wananchi (FDCs) kuhamishiwa katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mwaka 2016/2017 Wizara imeanza kufanya tathmini kwa vyuo vyote ili kujua mahitaji halisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutimiza azma hiyo, katika bajeti ya maendeleo kwa mwaka fedha 2017/2018 zimetengwa kiasi cha shilingi bilioni 12 kwa ajili ya kukarabati majengo na miundombinu ya baadhi ya Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi. Wizara pia katika bajeti ya maendeleo ya mwaka 2017/2018 imetenga shilingi bilioni 10 kupitia Mradi wa Kukuza Stadi za Kazi (ESPJ) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia na ambao utadumu kwa miaka mitano kuanzia mwaka 2017 imepanga kuviboresha kwa awamu vyuo hivyo 55 vya Maendeleo ya Wananchi, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi cha Sikonge kitatembelewa ili kuona uwezekano wa kukiboresha.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itakifanyia tathmini ya kina (ex-post evaluation) Kituo cha Vijana cha TULU kilichopo Sikonge?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Kituo cha Vijana cha TULU kinamilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge chini ya usimamizi wa Serikali ya Mkoa wa Tabora. Kilianzishwa mwaka 2014 kwa lengo la kuwawezesha vijana kupata mafunzo na stadi za ujuzi mbalimbali kama vile ujasiriamali, kilimo pamoja na ujenzi wa makazi bora. Baadaye vijana waanzilishi wa kituo hiki walikisajili kama asasi isiyo ya kiserikali (NGO) ijulikanayo kama Pathfinder. Baada ya kituo hiki kusajiliwa kama NGO, ilibainika kuwanufaisha vijana wachache tofauti na malengo yaliyokusudiwa ambayo ni kuwanufaisha vijana walio wengi ndani na hata nje ya Mkoa wa Tabora.
Mheshimiwa Spika, kutokana na kituo hiki kuendeshwa kwa maslahi ya vijana wachache, Serikali iliamua kuchukua hatua ya kubadili usajili wa kituo hiki kutoka kwenye NGO na kuwa kituo cha vijana kitakachosimamiwa na Serikali kwa lengo la kunufaisha vijana wengi zaidi. Aidha, nyaraka muhimu zimewasilishwa kwa mamlaka husika kwa ajili ya kubadilisha usajili huo wa awali. Baada ya maamuzi hayo kukamilika, Serikali itafanya tathmini ya kina ili kubainisha matumizi na programu mbalimbali zitakazotolewa katika kituo hiki.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Upembuzi yakinifu kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami barabara ya Ipole - Lungwa ulianza miaka mingi iliyopita na hii ni sehemu ya barabara kuu (trunk road) inayounganisha makao makuu ya Mkoa wa Mbeya. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 barabara hiyo imetengewa shilingi 350,000,000 kwa ajili ya kumalizia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwa ni pamoja na uandaaji wa nyaraka za zabuni kwa barabara ya Ipole hadi Lungwa yenye urefu wa kilometa 172 inaendelea. Katika mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi milioni 1,211 zimetengwa na katika mwaka wa fedha wa 2017/2018, tunashukuru mmezipitisha shilingi milioni 435 kwa ajili ya kukamilisha kazi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukamilika kwa upembuzi yakinifu, usanifu wa kina pamoja na maandalizi ya nyaraka za zabuni na gharama za mradi kujulikana, Serikali itaanza kutafuta fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Ipole hadi Lungwa.
MHE. ALMAS A. MAIGE (K.n.y. MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) aliuliza:-

Utalii wa uwindaji, utalii wa picha na ufugaji wa mapori ya misitu na Hifadhi ya Ugunda, Isuvangala na Ipembampazi ni miongoni mwa fursa kuu za utalii kwenye Jimbo la Sikonge:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Uwanja wa Ndege uliokuwa umeanza kujengwa karibu na Mlima wa Ipole ambao ulijumuisha pia ujenzi wa nyumba za kufikia watalii (tourist rest houses) kwenye Kijiji cha Ugunda?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imeendelea kuimarisha miundombinu katika maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini ili yaweze kufikika kwa urahisi na muda wote wa mwaka. Lengo kuu ni kuwezesha watalii kuyafikia maeneo hayo na hivyo kuiongezea mapato Serikali. Aidha, katika kuimarisha ulinzi wa rasilimali za wanyamapori katika Pori la Akiba Ugalla, mwaka 2005, Wizara ilifanya maandalizi ya ujenzi wa uwanja mdogo wa ndege (airstrip) karibu na Milima ya Ipole. Kazi ya awali iliyofanyika ikiwa ni maandalizi ya kutengeneza uwanja husika ilikuwa ni kuweka mipaka kwa kufyeka miti.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2006, Wizara ya Maliasili na Utalii iliomba Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ifanye tathmini ya eneo hilo ili kuona kama linakidhi vigezo vinavyotakiwa kwa mujibu wa sheria. Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ilibaini kuwa eneo pendekezwa lipo katikati ya milima na hivyo kupelekea usalama kuwa mdogo kwa ndege kutua na kuruka. Kutokana na ushauri huo, Wizara ya Maliasili ilisitisha maandalizi ya ujenzi wa uwanja husika na kujikita zaidi kuimarisha viwanja vilivyopo ndani ya Pori la Akiba Ugalla.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-

(a) Je, ni sababu zipi zinazosababisha matangazo ya Shirika la Habari Tanzania (TBC) hasa upande wa Radio yasisikike kwenye Tarafa za Kitunda na maeneo mengi ndani ya Jimbo la Sikonge?

(b) Je, ni lini Serikali itarekebisha tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako kwanza naomba nitumie fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuipongeza Timu yetu ya Taifa, Taifa Stars, kwa kutuheshimisha sisi kama Taifa kwa kuitoa Timu ya Burundi kwa mikwaju ya penati na hatimaye kuweza kutinga kwenye hatua ya makundi.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye swali; kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, TBC kwa Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2016/2017 ilitekeleza mradi wa upanuzi wa usikivu katika wilaya tano zilizopo mipakani mwa nchi yetu; wilaya hizo ni pamoja na Wilaya ya Longido Mkoani Arusha, Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro, Wilaya ya Tarime Mkoani Mara, Wilaya ya Nyasa Mkoani Ruvuma na Wilaya ya Kibondo Mkoani Kigoma. Aidha, Bajeti ya Mwaka 2017/2018 TBC ilitekeleza mradi wa upanuzi wa usikivu katika Mkoa wa Mtwara na Wilaya ya Lushoto Mkoani Tanga. Hadi kufikia tarehe 04 Mei, 2019 shirika lina vituo 33 vya kurushia matangazo katika masafa ya FM kwenye wilaya 102.

Mheshimiwa Spika, TBC inaendelea na mpango wa kupanua usikivu maeneo yote ya nchi nzima, kutegemeana na upatikanaji wa fedha ili kukamilisha wilaya zote 59 ikiwepo Wilaya ya Sikonge. Aidha, TBC ina mpango wa kufanya maboresho katika mitambo yake iliyopo Tabora Kaze Hill kisha kufanya tathmini ya usikivu na kubainisha maeneo yanayopaswa kufungiwa mitambo mingine ili kuleta usikivu Mkoa mzima wa Tabora ikiwepo Wilaya ya Sikonge.

Mheshimiwa Spika, katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2019/2020, TBC inaendelea kutekeleza mradi wa upanuzi wa usikivu katika maeneo ya Mikoa ya Unguja, Pemba, Simiyu, Njombe, Songwe pamoja na Lindi. Mkakati wa Serikali ni kuiwezesha TBC kufikia usikivu katika maeneo yote ya Tanzania.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-

Baadhi ya minara ya simu ya Vodacom, Airtel, Tigo na Halotel katika Kata za Kipili, Kilumbi, Kiloli, Kitunda, Kisanga, Mole, Kiloleli na Ipole haifanyi kazi vizuri kwani mtandao katika Kata hizo ni mdogo sana na hivyo wananchi hawapati huduma nzuri ya mawasiliano licha ya uwepo wa minara hiyo. Aidha, katika Kata za Nyahua, Igigwa na Ngonjwa hakuna kabisa mawasiliano ya simu:-

(a) Je, ni lini Serikali itawapatia mawasiliano ya uhakika wakazi wa Sikonge wanaoishi kwenye Kata zenye minara ya simu lakini isiyokamata mtando vizuri?

(b) Je, Serikali itawapatia lini mawasiliano ya simu wananchi wa Sikonge ambao wanaishi kwenye Kata ambazo hazina kabisa minara ya mawasiliano ya simu?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote imetoa ruzuku kwa ajili ya ujenzi wa minara ya mawasiliano katika Wilaya ya Sikonge katika Kata za Kiloli, Igigwa, Kipanga, Kipili na Kitunda kwa kushirikiana na TTCL na VODACOM kupitia miradi ya mawasiliano ya awamu ya kwanza na awamu ya tatu.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Igigwa, Serikali kupitia Mfuko ilitangaza zabuni na kupata mtoa huduma TTCL ambaye ameanza maandalizi ya ujenzi wa mnara katika kata hiyo. Kwa upande wa Kata za Nyahua na Ngonjwa, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote itazijumuisha kata hizi katika Mradi wa Mawasiliano Vijijini awamu ya tano ndani ya mwaka wa fedha 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) itafanya ukaguzi wa ubora wa huduma za mawasiliano kwa kushirikiana na watoa huduma kulingana na viwango vya ubora vilivyowekwa kwa mujibu wa Kanuni za Ubora ili kuhakikisha wananchi wanapata mawasiliano ya uhakika kwa maeneo yenye usikivu hafifu.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-

Je, ni kwa nini Serikali haitumii risiti za kielektroniki inapotoza faini za kuingiza mifugo kwenye Hifadhi zilizopo Sikonge?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu ya Sheria ya Wanyamapori Na.5 ya Mwaka 2009, ni kosa kwa mtu yeyote akiwemo mfugaji kuingiza mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa. Serikali iliweka sheria hii sio kwa ajili ya kujipatia mapato bali kudhibiti uharibifu ikiwemo uvamizi, ujangili na uingizaji wa mifugo ndani ya maeneo hayo kwa lengo la kuyatunza.

Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kudhibiti upotevu wa mapato, Serikali ilianzisha mfumo wa TEHAMA kwa ajili ya utoaji wa leseni au vibali, ukusanyaji wa takwimu na mapato ya vyanzo mbalimbali vya Sekta ya Maliasili na Utalii unaoitwa MNRT Portal ambao umefungamanishwa na Mfumo wa Government electronic Payment Gateway yaani GePG kwa ajili ya kutoa Control Number inayomwezesha mteja sasa yeyote yule kulipa. Aidha, baada ya kufanya malipo hayo mfumo wa MNRT Portal unatoa risiti ambazo zinatambulika na Mamlaka ya Mapato Tanzania yaani TRA.

Mheshimiwa Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa risiti zinazotolewa na mfumo huu ni halali kwa malipo ya Serikali sawa na zinazotolewa na mfumo wa Electronic Fiscal Devices yaani EFDs.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kusamehe kodi za miaka ya nyuma Taasisi za Dini zilizokuwa zikiendeshwa kwa utaratibu usiolenga kupata faida na kuziwekea utaratibu Taasisi hizo kuanza kulipa tangu walipojulishwa kutakiwa kulipa kodi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri Wa Ardhi, Nyumba Na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kudhibiti na kukabiliana na ujenzi holela mijini wizara imeandaa program ya utambuzi upangaji na umilikishaji wa ardhi yote katika kipindi cha miaka kumi, aidha katika bajeti ijayo wizara kwa kushirikiana na mamlaka za upapangaji imetenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mkakati ya utambuzi na upangaji upimaji na umilikishwaji wa ardhi nchini.

Mheshimiwa Spika, rai yangu kwa mamlaka zote 184 za upangaji kuendelea kutenga bajeti ya kutosha ili kuongeza kasi ya upangaji upimaji na umilikishaji wa ardhi ili kuwa na maeneo mengi yaliyopimwa ili kukabiliana na tatizo sugu la ujenzi holela. Ubunifu wa mbinu mpya ya upimaji ambayo ni shirikishi inayotumia teknolojia rahisi ya simu janja imeongeza kasi na usahihi wa kuimarisha majira nukta kwa kutumia GPS yaani Global Position System.

Mheshimiwa Spika, dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2023 maeneo yote yaliyoendelezwa bila kufuata taratibu za ujenzi mjini yawe yametambuliwa na kurasimishwa ambako program ya urasilimishaji ya miaka kumi yani 2013 mpaka 2023 itakuwa imefikia ukomo.

Mheshimiwa Spika, nizitake mamlaka zote za upangaji waongeze kasi ya utambuzi wa maeneo ambayo hayajaendelezwa kwa ajili ya kuyapanga na kuyapima na hivyo ujenzi holela mjini kukoma.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizi ofisi ya Rais- TAMISEMI pia inatekeleza program ya uboreshaji mfumo wa udhibiti wa ujenzi holela mijini Development Control strategic Program kwa kushirikiana na benki ya dunia. Program hii itawezesha mamlaka zote kuanzia ngazi ya mtaa kusimamia kudhibiti uendelezaji holela na kutoa taarifa za uendelezaji unaokiuka taratibu za ujenzi mijini ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itazalisha mbegu za mti wa mninga ili wananchi waweze kupanda na kuzalisha miti hiyo kibiashara?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umaarufu wa mti wa mninga katika matumizi ya shughuli za ujenzi na utengenezaji wa samani. Kutokana na umuhimu huo, Wizara kupitia TFS imeandaa mpango wa miaka mitano wa kuendeleza mti huo na miti mingine kibiashara kwa kuipanda kama ilivyo miti ya kigeni. Mpango huo unahusisha aina 56 za miti ya asili ikiwemo mninga ambapo kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 Wizara imetenga shilingi 60,000,000 kwa ajili ya kuzalisha mbegu za miti hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nia ya Wizara ni kuongeza kasi ya uzalishaji wa mbegu za miti ya asili ili wananchi waweze kuzipata kwa urahisi kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania zilizopo kwenye kanda mbalimbali hapa nchini. Aidha, Wizara itaendelea kuimarisha elimu ya upandaji wa mti wa mninga ili kuleta hamasa ya kupanda na kutunza miti hiyo. Serikali itahakikisha elimu ya utunzaji na uendelezaji wa miti ya mninga iliyopo katika maeneo ya mashamba ya wananchi inatolewa ili miti hiyo itunzwe kwa ajili ya kuzalisha mbegu ili kuwezesha wananchi kupanda miti ya mninga kibiashara.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo sugu la soko la zao la tumbaku nchini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, soko la tumbaku linategemea mahitaji katika soko la dunia. Mahitaji ya tumbaku na bidhaa zake yamekuwa yakishuka katika Soko la Dunia kwa wastani wa asilimia sita hadi saba kwa mwaka. Hali hiyo inachangiwa kwa kiasi kikubwa na kampeni ya kidunia ya kupunguza uzalishaji na matumizi ya tumbaku pamoja na bidhaa zake, pamoja kuanza matumizi ya sigara aina mpya inayotumia kilevi cha kutengeneza maabara (Laboratory nicotine) iitwayo e-cigarette.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Bodi ya Tumbaku Tanzania inaendelea kutafuta masoko ya tumbaku kwa kuwashawishi wanunuzi waliopo kuongeza kiwango cha ununuzi kwa njia ya mkataba, kutafuta wanunuzi wapya na pia kutafuta masoko mengine mapya nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kufuatia hatua hizo, wanunuzi wakubwa wameongeza ununuzi wa tumbaku kutoka kilo 39,000,000 katika msimu wa mwaka 2017/2018 hadi kilo 57,000,000 msimu wa mwaka 2021/2022, sawa na ongezeko la asilimia 46. Serikali imehamasisha wanunuzi wapya na kwa msimu wa 2021 kampuni nane za kizawa zilingia mkataba na wakulima kununua kilo 17,000,000. Katika hatua nyingine Serikali imeendelea kutafuta masoko mapya ambapo, Serikali inaendelea kutafuta soko la China na tayari walileta aina ya tumbaku wanayotaka na majaribio yamefanyika na sampuli ya tumbaku hiyo imepelekwa kwa hatua zaidi.

Mheshimiwa Spika, jitihada za kutafuta masoko zinaendelea katika nchi mbalimbali, Serikali inaamini kuwa baada ya muda mfupi tatizo la soko kwa wakulima wa tumbaku wa Tanzania linaenda kupungua.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Uwanja wa Ndege wa Ipole pamoja na nyumba ya kupumzikia wageni wanaokuja kwa ajili ya utalii wa picha na kuangalia Wanyama kwenye WMA ya JUHIWAI, Mbuga za Ipembampazi na Isuvangala utajengwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa wageni wanaokwenda Ipole WMA kufanya shughuli za utalii wanatumia uwanja wa ndege wa Tabora, pamoja na kiwanja kidogo cha Koga kilichopo katika eneo la WMA. Hata hivyo, Serikali itaendelea kuhamasisha wawekezaji wanaowekeza katika maeneo hayo kujenga uwanja wa ndege pamoja na nyumba ya kupumzikia wageni ili kuhakikisha wageni wanaokwenda kwenye WMA ya Ipole, Mbuga za Ipembampazi na Isuvangala kwa ajili ya utalii wanaofika katika eneo husika bila tatizo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga shule mpya za msingi katika maeneo ya Mbirani, Makibo, Kiyombo na Tutuo – Sikonge?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI inakamilisha tathmini ya upembuzi yakinifu wa Shule zote za msingi kupitia mradi wa Boost ili kubaini taarifa za eneo shule ilipo, hali ya mazingira shule ilipo, umbali kutoka shule moja hadi nyingine, umbali kati ya shule na makazi ya watu na idadi ya watu (School Mapping). Lengo lake likiwa ni kuandaa mpango endelevu wa uboreshaji wa elimu nchini.

Mheshimiwa Spika, baada ya uhuishaji huo, kwa mwaka wa fedha 2022/2023 kupitia mradi wa Boost Serikali imetenga Shilingi Bilioni 230 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya shule za msingi katika Halmashauri zote 184 ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni kwa nini Serikali isitoe matibabu bure kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Matibabu ya watoto chini ya miaka mitano wenye matatizo ya kiafya ikiwemo Selimundu ni bure kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2007. Hivyo utambuzi na matibabu ya watoto wenye tatizo la selimundu hutolewa bila malipo.

Mheshimiwa Spika, suluhisho la tatizo hili ni Bima ya Afya kwa Wote.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali isipitishe mkakati maalum kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023 wa kujenga shule za msingi kwenye vitongoji vyote vyenye watoto zaidi ya 200?

NAIBU WAZIRI, OFISI RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ya Serikali ni kuwa na Shule ya Msingi kila Kijiji ikiwemo na vitongoji katika jimbo la Sikonge.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ukweli kuwa Jimbo la Sikonge kwa sasa halina shule za msingi za kutosha, Halmashauri ya Sikonge kupitia fedha toka Serikalini na kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya mapato vya Halmashauri inaendelea kuhimiza wananchi, jamii na wadau wa maendeleo kujenga miundombinu ya shule za msingi ili kukidhi mahitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kutenga fedha kwa ajili ya kujenga shule za msingi kila kitongoji kutategemeana na hali ya uchumi wa nchi na upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, kwa jinsi sera ilivyo hatujafikia hatua ya kujenga shule kwa kila kitongoji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa shughuli ya ujenzi wa shule inawahusisha wananchi na jamii kwa ujumla, napenda kumshauri Mheshimiwa Mbunge kuendelea kushirikiana na wananchi na Halmashauri kujenga shule katika kila kijiji ili kuwezesha wanafunzi wote wenye umri wa kwenda shule kuweza kupata nafasi.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Wananchi wa Sikonge watapatiwa eneo la hekta 33,000 kwenye Mbuga ya Ipembampazi litumike kwa kilimo na ufugaji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Msitu wa Ipembampazi ina umuhimu katika kuimarisha mfumo wa ikolojia wa Ugalla - Moyowosi unaojumuisha maeneo ya hifadhi yaliyopo katika Mikoa ya Tabora na Kigoma ambapo eneo la msitu huo linatumika kama mtawanyiko na mapito ya wanyamapori hususan tembo. Eneo hilo lina wanyamapori wa aina mbalimbali na limetengwa kuwa kitalu cha uwindaji wa wenyeji.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka alama za mipaka kutenganisha maeneo ya hifadhi na vijiji 975 vilivyotolewa kwenye Hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kuweka alama za mipaka kutenganisha maeneo ya Hifadhi na Vijiji 975 vilivyotolewa kwenye hifadhi imefanyika katika baadhi ya hifadhi na bado kazi hiyo inaendelea. Hifadhi zilizowekewa alama za mipaka mpaka sasa ni pamoja na eneo la kilomita za mraba 1,500 za Hifadhi ya Pori Tengefu Loliondo vigingi 422 vya alama vilishawekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Pori la Akiba la Wamimbiki alama 277 na kilomita 156 za mkuza zimetengenezwa. Hifadhi ya Pori la Akiba Swagaswaga alama 226 kati ya 250 na kilomita 27 za mkuza zimetengezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Pori la Akiba Mkungunero alama 99 kati ya 157 na kilomita 35.8 za mkuza zimetengenezwa. Hifadhi ya Taifa ya Ruaha alama 650 na kilomita 177 za mkuza zimeishatengenezwa pamoja na Bonde la Usangu, alama 632 zimewekwa kwenye eneo lenye urefu wa kilomita 316 kati ya 350 na mkuza wenye kilomita za mraba 177 umechongwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoani Tabora, alama za mipaka zimeshawekwa kwenye vijiji vitano vya Mwendakumila, Mwaharaja, Chemkeni, Uhindi na Nsimbo vya Wilaya ya Kaliua vilivyokua kwenye hifadhi ya Ulyankulu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa kwa kushirikiana na Taasisi zinazohusika na usimamizi wa hifadhi, kuendelea na utekelezaji wa uamuzi wa Baraza la Mawaziri ikiwemo kazi ya kuweka mipaka kwa kutumia alama za kudumu zinazoonekana ili kuimarisha ulinzi katika maeneo hayo, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza kazi ya kuwapatia wananchi Vitambulisho vya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kazi ya kuwapatia wananchi Vitambulisho vya Taifa ni endelevu kwa kuwa kila mwaka kuna wananchi wanaotimiza umri wa miaka 18 ambao wanastahili kupewa Vitambulisho vya Taifa. Aidha, wapo wananchi wanaopoteza vitambulisho au wenye vitambulisho vinavyoharibika na hivyo kuhitajika vingine.

Mheshimiwa Spika, wananchi ambao walitambuliwa lakini hawajapata vitambulisho vyao, Serikali inatarajia kuwapatia vitambulisho vyao ifikapo mwezi Machi, 2024, nashukuru.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Halmashauri ya Sikonge itapatiwa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kujenga Vituo vya Afya Ipole, Kipanga na Usunga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilitenga shilingi milioni 500 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Tutuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuweka mipango Madhubuti ya ujenzi wa vituo vya afya vikiwemo vituo vya afya vya Ipole, Kapanga na Usunga ili kuendelea kutoa na kuboresha huduma za afya nchini.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, lini Serikali itafanya marekebisho ya Sheria ya Usalama Barabarani ili kuweka tozo tofauti kulingana na ukubwa wa chombo cha moto?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kufanya marekebisho na kuiboresha Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168 ya mwaka 1973 kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002. Kwa sasa Serikali inaendelea kuboresha Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Usalama Barabarani ambao tayari ulishasomwa kwa mara ya kwanza hapa Bungeni. Pamoja na mambo mengine, mswada huo umezingatia mahitaji ya sasa ikiwa ni pamoja na kuweka viwango tofauti vya tozo kulingana na ukubwa wa chombo cha moto kama Mheshimiwa Mbunge anavyoshauri, nashukuru.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, nyumba bora ya kuishi inatakiwa kuwa na sifa zipi na ni kwa nini Serikali haiweki ruzuku kwenye vifaa vya ujenzi?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kumjibu Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge na Chifu wa Wakonongo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nyumba ni mojawapo ya mahitaji muhimu ya mwanadamu. Nyumba bora ni ile yenye huduma bora kwa usalama na afya kwa wakazi wake. Jitihada za Serikali kuhakikisha nyumba bora zinajengwa kwa gharama nafuu ni pamoja na kuweka mazingira wezeshi ya uanzishwaji wa viwanda vya kuzalisha vifaa vya ujenzi, kufanya utafiti na kuwezesha matumizi ya teknolojia ya kisasa katika kazi za ujenzi na kuhamasisha taasisi za fedha kutoa mikopo kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na ununuzi wa nyumba.