Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Joseph George Kakunda (72 total)

MHE. BONIPHACE M. GETERE (K.n.y. MHE. AMINA N. MAKILAGI) Aliuliza:-
Wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma katika Kata za Etaro, Ifulifu, Nyegina na Nyakatende wanakabiliwa na taizo la maji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wananchi wa kata hizo maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Amina Makilagi naomba kwanza nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa aliyoionyesha kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais , TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassor Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma katika Kata za Itaro, Ifulifu, Nyegina na Nyakatende wanakabiliwa na tatizo la maji kwa sababu mahitaji halisi ya maji katika kata hizo ni lita 953,550 wakati uzalishaji wa maji katika vyanzo vilivyopo ambavyo ni visima sita katika Vijiji vya Keimba na Kabegi kwenye Kata ya Ifulifu, Kijiji cha Mkikira katika Kata ya Nyegina na Vijiji vya Kigera, Nyegina na Kamguruki katika Kata ya Nyakatende vinazalisha lita 5,100 kwa siku pamoja na mradi wa maji ya bomba katika Kata ya Nyegina unazalisha lita 50,000 kwa siku na hivyo kufanya jumla ya lita zinazozalishwa kwa sasa kuwa 55,100 tu ambazo ni asilimia sita ya mahitaji.
Mheshimiwa Spika, katika juhudi za kuboresha huduma za maji kwenye eneo hilo, Serikali inakamilisha ujenzi wa mradi mkubwa wa maji utakaohudumia wakazi wa Manispaa ya Musoma pamoja na wakati wa Kata za Nyamkanga, Bukabwa na Busimwa katika halmashauri ya Wilaya ya Butiama na wakazi kwenye Kata za Etaro, Nyegina na Nyakatende katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma. Hadi sasa Serikali imeshapeleka shilingi milioni 900 kwenye Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Musoma, ambayo inasimamia utekelezaji wa mradi huo.
Mheshimiwa Spika, kazi ambazo zimeshatekelezwa hadi sasa ni kupima njia ya bomba, kuchonga barabara kuelekea Mlima Balima kutakakojengwa tenki lenye ujazo wa lita milioni mbili ambalo litasambaza maji kwa mtiririko kupeleka huduma za maji safi na salama katika kata nilizotaja. Aidha, taratibu za ununuzi wa mabomba yenye urefu wa kilometa 35 zimekamilika.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-
(i) Je, Serikali ina mkakati gani mahususi katika kuboresha mazingira ya kujifunza katika shule za umma za sekondari nchi nzima ikiwa ni pamoja na ukarabati wa majengo, madarasa, mabweni na maabara?
(ii) Je, kwa nini Serikali isione umuhimu wa kuifuta kazi Bodi na Menejimenti ya Mamlaka ya Elimu Tanzania na kuiunda upya kwa sababu imeshindwa kusimamia ubora wa elimu nchini?
(iii) Je, Serikali ina mpango gani wa kuzifufua shule zilizokuwa za watoto wenye vipaji maalum?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), refu sana, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia katika shule za umma za sekondari nchini. Kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES II) ulianza kutekelezwa mwaka 2004 hadi mwezi Disemba 2016, jumla ya shule za sekondari 792 zimejengwa na kukarabatiwa miundombinu yake na kuwa shule kamili kwa gharama za shilingi bilioni 123.8.
Aidha, katika kipindi hicho jumla ya maabara 6,287 sawa na asilimia 60.52 ya lengo zimekamilika kati ya maabara 10,387 zilizohitajika. Kupitia Mpango wa Lipa kwa Matokeo kwa mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya shilingi bilioni 21.9 zimeidhinishwa kwa ajili ya upanuzi wa shule 85 za sekondari na shule 19 za msingi. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya vyumba vya madarasa 320, mabweni 155 yenye uwezo wa kulaza wanafunzi 80 kila moja na matundu ya vyoo 829 yatajengwa.
(b) Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Elimu Tanzania huchangia katika kukuza ubora wa elimu nchini kupitia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta ya elimu kuanzia ngazi ya elimu ya awali hadi chuo kikuu. Changamoto iliyopo ni upatikanaji wa fedha za kutosha kuwezesha kutekeleza miradi mingi zaidi kama inavyotarajiwa na wananchi katika maeneo mengi nchini.
(c) Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuzikarabati shule kongwe 89 zikiwemo shule nane za wanafunzi wenye vipaji maalum kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania na Mpango wa Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R). Mradi huu utakaogharimu jumla ya shilingi bilioni 89 hadi kukamilika unatekelezwa kwa awamu. Hadi kufikia Julai, 2017 jumla ya shule kongwe 43 zimekarabatiwa na shule 20 zitakarabatiwa katika mwaka wa fedha 2017/2018.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza:-
Ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Morogoro umekamilika lakini haina umeme wala maji:-
Je, ni lini Serikali itapeleka umeme na maji katika hospitali hiyo ili ianze kutumika na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Morogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dokta Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya mifumo ya umeme na maji katika Hospitali mpya ya Wilaya ya Morogoro. Ifikapo tarehe 15 Novemba, 2017, Sh.25,240,969.33 zitakuwa zimelipwa kwa ajili ya kuingiza umeme hospitalini hapo. Hadi sasa TANESCO wameshaweka nguzo na mfumo wa umeme katika jengo la hospitali, kazi iliyobaki ni kufunga transfoma ili umeme uweze kuwashwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu ya maji hospitalini hapo utakaogharimu shilingi milioni 50 unaendelea. Kati ya hizo, shilingi milioni 21 zimeshapelekwa kulipia kazi zinazoendelea. Mifumo ya huduma ya maji itakuwa imekamilika ifikapo mwishoni mwa Januari, 2018.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-
Kijiji cha Mtisi katika Kata ya Sitalike hakuna eneo la kilimo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapa wananchi hao maeneo kwa ajili ya kilimo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Mtisi kilichopo katika Kata Sitalike, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kina eneo la ardhi lenye jumla ya hekta 1,066.86. Kati ya hizo, hekta 1,043.86 ni sehemu ya Hifadhi ya Msitu wa Msaginya unaomilikiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS). Maana yake ni kwamba, jumla ya kaya 589 zenye wakazi 3,416 wa kijiji hicho wamebakia na eneo la hekta 23 tu wanaloruhusiwa kulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mahitaji ya ardhi ya kilimo katika kijiji hicho ni hekta 919.4, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, ifikapo mwishoni mwa Novemba, 2017, itakuwa imewapatia ardhi wakazi hao kutoka katika Kijiji cha Stalike (Makao Makuu ya Kata ya Sitalike) chenye ardhi ya ziada hekta 2,950.
MARWA R. CHAHA (K.n.y. MHE. SABREENA H. SUNGURA) aliuliza:-
Akiwa katika Kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka 2025 Mheshimiwa Rais aliahidi ujenzi wa barabara ya lami (Kasulu Road) ili kufungua Mji wa Ujiji:-
Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Hamza Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania aliahidi ujenzi wa kilomita10 za barabara kwa kiwango cha lami ndani ya Manispaa ya Kigoma Ujiji. Kutokana na ahadi hiyo, Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji imeamua kujenga barabara ya Ujiji
– Bulenga - Bangwe yenye urefu wa kilomita 7.5 ambapo usanifu umekamilika na itagharimu shilingi bilioni 11.6 ambapo ujenzi unaweza kuanza mwaka wa fedha 2018/2019 na barabara ya Ujiji hadi Daraja la Mngonya yenye urefu wa kilomita 2.5, hivyo kufanya jumla ya kilomita10 ambazo Mheshimiwa Rais aliahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ili uunganishe na ile barabara ya kutoka Kasulu lazima upembuzi yakinifu na usanifu wa barabara hiyo ufanyike kuunganisha kutoka Daraja la Mungonya hadi barabara Kigoma - Kasulu katika eneo la Msimba lenye urefu wa kilomita tatu. Kipande hicho cha kutoka Daraja la Mngonya hadi Msimba hakijafanyiwa upembuzi yakinifu. Kwa hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma inashauriwa kuweka kipaumbele na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara kutoka Daraja la Mto Mngonya hadi Msimba kwa kiwango cha lami.
RUTH H. MOLLEL aliuliza:-
Maboresho ya utendaji wa Serikali za Mitaa yalilenga kuimarisha na kujenga uwezo wa Serikali za Mitaa kujiendesha kwa kuwapatia rasilimali watu na fedha za kutosha kutekeleza Sera ya Ugatuaji wa Madaraka.
Je, Serikali ina lengo gani kuimarisha Serikali za Mitaa ziweze kujiendesha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ibara za 145 na 146 za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mamlaka za Serikali za Mitaa ni mamlaka shirikishi za kisheria na kidemokrasia zilizoanzishwa kwa kwa lengo la kuwashirikisha wananchi katika shughuli zote za maendeleo, huduma za jamii, utawala bora, utekelezaji wa sheria, ulinzi na usalama kwa kuzingatia kanuni za uwazi na uwajibikaji.
Mheshimiwa Spika, tangu mwaka 1999 Serikali imetekeleza programu mbalimbali za kuboresha utendaji katika ngazi ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Miongoni mwa programu hizo ni Programu ya Maboresho ya Serikali za Mitaa iliyolenga kuimarisha miundo na mifumo ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ili zijiendeshe na kuwahudumia wananchi kwa ufanisi. Aidha, Programu ya Maboresho ya Usimamizi wa Fedha imeimarisha na kuinua uwezo wa Halmashauri katika kukusanya mapato na kudhibiti matumizi.
Mheshimiwa Spika, katika kuziimarisha zaidi Mamlaka za Serikali za Mitaa, bajeti ya ruzuku ya maendeleo kwa Halmashauri imeongezeka kutoka shilingi bilioni 49 mwaka 2008 hadi shilingi bilioni 249 mwaka 2017. Aidha, kuanzia mwaka 2015, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeruhusiwa kwa mujibu wa sheria kuajiri watumishi wake wa kada 22 za ngazi za chini ikiwemo Watendaji wa Vijiji baada ya kupata kibali cha kuajiri. Ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Wilaya za Kakonko, Buhigwe na Uvinza ni Wilaya mpya ambazo hazina Hospitali za Wilaya.
Je, ni lini Serikali itajenga Hospitali za Wilaya katika Wilaya hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko imeidhinishiwa jumla ya shilingi milioni 500 kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Ujenzi wa hospitali hiyo unatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 1.5 hadi kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza imetenga eneo la ekari 80 na imekamilisha michoro ya jengo la Hospitali ya Wilaya. Halmashauri imeshauriwa kuweka kipaumbele na kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2018/2019 ili kuanza ujenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Wilaya kwa kuanza na jengo la wagonjwa wa nje, utawala na maabara unaogharibu shilingi milioni 450. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri imetengewa shilingi milioni 500 kuendelea na ujenzi. Kazi hii inatekelezwa na SUMA JKT na kazi inaendelea. Ujenzi wa hospitali unafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha na unakadiriwa kugharimu shilingi bilioni 6.4 hadi kukamilika.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y MHE. YOSEPHER F. KOMBA) aliuliza:-
Ni dhamira ya Serikali kutekeleza mpango wa elimu bure kuanzia chekechea hadi kidato cha nne, lakini mpango huu una changamoto ambazo zisipotatuliwa zitasababisha kushuka kwa ubora wa elimu.
(a) Je, ni nini tamko la Serikali juu ya wanafunzi wanaoanza kidato cha kwanza kwa kigezo cha kutofaulu kwa kiwango cha kianzia alama 100 na kuendelea?
(b) Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha ujenzi wa maabara unakamilika kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tamko la Serikali ni kwamba mwanafunzi anahesabiwa kufaulu mtihani wa Taifa wa darasa la saba endapo atapata alama kuanzia 100 hadi 250 katika masomo yote aliyoyafanya. Hata hivyo, wanafunzi walio na alama chini ya 100 huhesabika kuwa ni miongoni mwa waliokosa sifa za kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wanafunzi walioshindwa kufikia alama 100 na kuendelea, hushauriwa kujiunga na mfumo usio rasmi wa Elimu Masafa (Open Distance Learning) unaosimamiwa na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, vyuo vya ufundi au shule za sekondari za binafsi. Wanafunzi wanaojiunga na mfumo huo wa elimu hawamo katika utaratibu wa utekelezaji wa mpango wa elimu msingi bila malipo, lakini wanafunzi wanaosoma katika utaratibu huo watakaofaulu mtihani wa Taifa wa kidato cha nne huchaguliwa kujiunga na kidato cha tano katika shule za Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la (b); ujenzi wa maabara katika Halmashauri zote unaendelea ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia masomo ya sayansi. Kati ya maabara 10,387 zinazohitajika nchini, ujenzi wa maabara 6,287 sawa na asilimia 60.5 ya mahitaji umekamilika.
Nazikumbusha Halmashauri zote kukamilisha mapema ujenzi unaoendelea kwa kushirikisha wadau na nguvu za wananchi.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaondoa vikwazo kandamizi kwa walimu wanaotaka kuhama vituo vyao vya kazi kwa hiari yao kutokana na sababu mbalimbali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna vikwazo kandamizi kwa walimu wanaotaka kuhama vituo vyao vya kazi kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kufuata wenza wao au ugonjwa. Hata hivyo, katika kuhamisha mwalimu, Serikali inazingatia ikama ili kutoathiri taaluma kwa kuhakikisha wanafunzi wanaendelea kufundishwa masomo yote kwa mujibu wa mitaala ya elimu iliyoidhinishwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mheshimiwa Naibu Spika, hitaji hilo ndiyo husababisha katika baadhi ya maeneo walimu kusubiri apatikane mwalimu mbadala kwanza kabla ya kutolewa kibali cha uhamisho ili wanafunzi wasikose haki yao ya kusoma masomo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kwamba uhamisho wa mtumishi wa umma ni haki yake endapo atazingatia utaratibu uliowekwa. Ndiyo maana kuanzia Julai, 2017 hadi sasa Serikali imetoa vibali vya uhamisho kwa walimu 2,755 nchi nzima. Aidha, taratibu za kutoa vibali vya uhamisho kwa walimu wengine walioomba uhamisho zinaendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuwaelekeza walimu nchi nzima na watumishi wengine wote kuzingatia utaratibu na waache kutumia viongozi mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wabunge kuwaombea uhamisho. (Kicheko)
MHE. JASSON S. RWEIKIZA aliuliza:-
Maeneo mengi ya Bukoba Vijijini kama vile Kata za Ruhunga, Kibirizi, Izimbya, Mugajwale, Rukoma, Kikomelo na nyingine yana tabu kubwa sana ya upatikanaji wa maji na kilio hiki kimekuwa cha muda mrefu sana:- Je, ni kwa nini Serikali haichukui hatua ya kuwasaidia wananchi hao.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jasson Samson Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hali ya upatikanaji wa huduma za maji kwenye maeneo aliyoyataja bado ni changamoto. Hata hivyo, kwa uhalisia hali hiyo ni tofauti na maeneo mengi ya Halmashauri ya Bukoba Vijijini ambako Serikali imekamilisha hivi karibuni miradi 18 ya maji kwenye Kata za Nyakibimbili, miradi mitatu (3); Kyamulaile, miradi mitatu (3); Kemondo, miradi mitatu (3); Buteragunzi, miradi minne (4); Rubole, mradi mmoja (1); Karabagaine, mradi mmoja (1); Rubafu (mradi mmoja (1); na Mikoni, miradi miwili (2) iliyogharimu shilingi 3,552,117,690 inayohudumia wakazi 61,279; hali hiyo imeinua upatikanaji wa maji hadi kufikia asilimia 64 ya upatikanaji wa maji kwa wakazi wote wa Bukoba Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya upatikanaji wa maji itapanda zaidi hadi kufikia asilimia 75 ifikapo mwezi Juni, 2018 kutokana na kukamilika kwa miradi ya Rukoma, Ubwera, Katoma na Kibirizi inayogharimu Sh.2,235,274,135 na itakayohudumia wakazi 18,449.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa kuna visima 75 vinavyofanya kazi kwenye Kata ya Rukoma, Ruhunga, Butulage, Mgajwale, Izimbya, Katoro, Rubale, Kaibanja, Kishogo, Kasharu, Maruku na Kikomero; na vyanzo vingine 90 vya maji kwenye Kata za Nyakato, Buhendagabo, Katerero na Bujugo. Serikali itatekeleza miradi ya maji kwenye Kata za Ruhunga, Mugajwale, Izimbya na Kikombero ambako kwa sasa wakazi wake wanahudumiwa na visima 23 vyenye uwezo wa kuhudumia watu 7,500 kati ya wakazi 11,794 waliopo katika Kata hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia awamu ya pili ya utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji kwa Mwaka 2018/2019 imetenga shilingi bilioni 2.5 endapo Bunge litaridhia ili kuboresha zaidi upatikanaji wa huduma za maji Bukoba Vijijini ikiwemo maeneo yaliyotajwa na Mheshimiwa Mbunge.
MHE. CECIL D. MWAMBE (K.n.y MHE. UPENDO F. PENEZA) aliuliza:-
Je, Serikali imeweka mikakati gani kuimarisha huduma za umeme, maji, afya na elimu katika maeneo ya vijijini ili kuongeza uzalishaji katika maeneo hayo na kuzuia wimbi la watu kukimbilia mijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Upendo Furaha Peneza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza uzalishaji katika maeneo ya vijijini kwa kuimarisha huduma za umeme, maji, afya na elimu kwa lengo la kuzuia wimbi la watu kukimbilia mijini Serikali inatekeleza mikakati ifuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, kuendelea kuboresha miundombinu ya shule za msingi na sekondari kwa kujenga na kukarabati madarasa, vyoo, maabara, mabweni, nyumba za walimu, mabwalo, maktaba kwa kuzingatia mahitaji ya shule husika. Pia kujenga shule mpya katika maeneo ambayo shule za msingi na sekondari ziko mbali. aidha, mkakati wa madawati kwa kila shule, mkakati wa kujenga maabara kwa shule za sekondari na ajira mpya kwa walimu wapya wa michepuo ya sayansi ni miongoni mwa mikakati mahususi ya kuboresha sekta ya elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili, kuendelea kuboresha miundombinu kwenye sekta ya afya ambapo kwa mwaka huu wa fedha pekee Serikali inajenga na kukarabati vituo vya afya 183 kwa gharama ya shilingi bilioni 81 vitakavyokamilika ifikapo tarehe 30/4/2018; ambapo shilingi bilioni 35.7 zimetolewa kwa ajili ya vifaa tiba. Ili kuongeza upatikanaji wa dawa Serikali imeongeza bajeti ya dawa kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015/2016 hadi shilingi bilioni 260 mwaka huu wa fedha 2017/2018 ambazo zimesaidia sana kuongeza upatikanaji wa dawa mijini na vijijini. Pia kipaumbele maalum kimewekwa kuhusu kuongeza watumishi wa afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya nishati vijiji 7,873 kati ya vijiji 12,545 vya Tanzania Bara vitapatiwa umeme kuanzia mwaka huu wa fedha 2017/2018 hadi 2021. Umeme utasambazwa hadi kwenye maeneo yote ya shule, zahanati, vituo vya zfya, hospitali, mitambo ya maji, viwanda vidogo vidogo, viwanda vya kati na viwanda vikubwa.
Aidha, huduma za maji zitaboreshwa zaidi kupitia utekelezaji wa awamu ya pili ya Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji. Serikali pia itaendelea kuimarisha barabara vijijini ili kupunguza gharama za usafiri na usafirishaji hasa wa mazao kwenda kwenye soko.
MHE. ALLY S. UNGANDO aliuliza:-
Maeneo ya Kibiti, Bungu, Jaribu Mpakani na Nyamisati katika Jimbo la Kibiti yanakuwa kwa haraka sana na kuongezeka kwa shughuli za kibinadamu.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupanga mipango miji?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mitandao na kuchonga barabara za mitaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Seif Ungando, Mbunge wa Kibiti lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti kwa mujibu wa Sheria Namba 8 ya Mipango Miji ya mwaka 2007 imeandaa Mpango Kabambe (Master Plan) wa Mji Mdogo wa Kibiti ili kuwa dira ya upangaji na uendelezaji wa mji huo ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Kibiti. Kazi hiyo imepangwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Februari, 2018 na kuwasilishwa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya kuidhinishwa na kusajiliwa. Michoro hiyo itakuwa na jumla ya viwanja 360 ambapo kati ya hivyo, viwanja vya matumizi ya makazi ni 205, makazi na biashara 82, viwanja vya matumizi ya umma 25, makazi maalum (housing estate) nane , viwanda vidogo 20 na maeneo ya wazi 20.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa miundombinu zikiwemo barabara ndani ya Mji Mdogo wa Kibiti utaanza kutekelezwa baada ya kuidhinishwa kwa michoro ya mipango miji na Wizara yenye dhamana na Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA aliuliza:-
Wilaya ya Karagwe ina walimu ambao bado wanadai malimbikizo ya mishahara, walimu hawa hupandishwa madaraja bila ya kurekebishiwa mishahara yao kitu ambacho kimekuwa ni kero kubwa kwa walimu wa Karagwe na maeneo mengine nchini.
(a) Je, Serikali inawaambia nini walimu hawa na imefikia wapi kutatua kero zao?
(b) Je, Serikali imefikia wapi katika kuhakikisha Teachers Service Commission (TSC) inapata rasilimali watu na fedha ili iweze kutetea maslahi ya walimu nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Lugha Bashungwa, Mbunge wa Karagwe lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikilipa madeni ya malimbikizo ya mishahara ya walimu kila mwezi kupitia akaunti zao za benki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia tarehe 30/6/2017 Serikali imelipa kiasi cha shilingi bilioni 14.236 kwa walimu 18,865 kati ya shilingi bilioni 69.461 ilizokuwa ikidaiwa hadi kipindi cha 2015/2016 ambapo walimu 12,284 ni wa shule za msingi na 6,581 ni wa shule za sekondari wakiwemo walimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe 105 waliolipwa jumla ya shilingi 110,555,836.70. Serikali itaendelea kuongeza kiasi inacholipa kwa mwezi ili kumaliza kabisa deni hili kwa muda mfupi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu TSC, Serikali imeendelea kuimarisha Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) kwa kuipatia Ofisi za Makao Makuu, Ofisi za Wilaya pamoja na kuipatia samani na watumishi katika ofisi hizo. Kwa mfano, Ofisi ya TSC Wilaya ya Karagwe yupo Katibu wa Wilaya na Maofisa wawili. Katika mwaka huu 2017/2018 TSC imepewa kibali cha nafasi za ajira mpya 26 na mwaka ujao 2018/2019 nafasi 43 endapo Bunge litaridhia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo ni kukamilisha ikama iliyoidhinishwa inayohitaji watumishi wasiopungua sita na wasiozidi nane kwa kila Wilaya. Hadi Desemba, 2017 TSC imepewa shilingi bilioni 1.247 za matumizi mengine ukiacha mishahara kati ya shilingi bilioni 4.622 zilizotengwa mwaka huu 2017/2018. Bajeti ya mishahara ikijumlishwa na hiyo Bajeti ya Matumizi Mengineyp (OC), TSC kwa mwaka 2017/2018 imetengewa jumla ya shilingi 12,422,291,495.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Hydom umechukua muda mrefu kumalizika na wananchi wanasubiri maji huku muda wa mkataba na mkandarasi ukiwa umeisha.
Je, kwa nini Serikali isimfukuze mkandarasi huyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji wa Mji wa Haydom ulianza kutekelezwa mwaka 2014 lakini kutokana na changamoto ya fedha utekelezaji ulisimama mwaka 2015/2016. Hata hivyo, pamoja na mkataba wa mkandarasi kuisha muda wake, napenda nimsifu na kumshukuru Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, kwa kushirikiana na Mkuu wa Wilaya Mheshimiwa Chelestino Mofuga na Mkurugenzi wa Halmashauri Ndugu Hudson Kamoga kwa kufanya kikao kati yao na mkandarasi chini ya Uenyekiti wa Katibu Mkuu wa Wizara ya maji Profesa Kitila Mkumbo tarehe 2/11/2017, ambapo muafaka wa mkandarasi kuendelea kutekeleza mradi huo unaotarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2018 ulipatikana. Kwa maana hiyo, wakazi wa vijiji vya Haydom na Ng’wandakw vinavyounda Mji wa Haydom wenye wakazi 17,406 wataanza kupata maji baada ya mradi huo kukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nyongeza yangu kuhusu taarifa tulizozipata usiku wa leo zinazohusu changamoto za Mkandarasi zinazohitaji utatuzi wa haraka namwomba Mheshimiwa Flatei Massay na mwenzangu Naibu Waziri wa Maji tukutane hapa Bungeni baada ya kipindi cha asubuhi ili tupate utatuzi wa haraka wa mradi huo. (Makofi)
MHE. PROF. NORMAN A. S. KING aliuliza:-
Mwaka 2013 Serikali ilianza kutekeleza mradi wa maji wa Kata za Kinyika na Matamba katika Wilaya ya Makete lakini mradi huo haukufanikiwa kutokana na Serikali kutoa maelekezo ya kulaza mabomba ya inchi 2.5 na 4 badala ya inchi 8 kwenye mradi wa kilometa 18; mradi wa maji wa Tarafa za Magoma na Bulongwa ulijengwa muda mrefu wakati idadi ya watu ikiwa ndogo lakini sasa idadi ya watu na matumizi vimeongezeka.
(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa mradi wa maji wa Tarafa ya Matamba?
(b) Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa maji wa Tarafa ya Bulongwa ili Kata za Bulongwa, Kipagalo na Luwumbu ziweze kupata maji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norman Sigalla King, Mbunge wa Makete lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji wa Kata ya Matamba na Kinyika unaosambaza huduma za maji kwenye vijiji tisa ulianza kujengwa mwaka 2007 na ulikamilika mwaka 2014. Kabla ya ujenzi kuanza usanifu wa mradi huo ulilazimika kubadilishwa ili kutumia bomba la inchi 4, 2 na 1.5 badala ya bomba la inchi 8 kulingana na fedha zilizokuwepo kwani gharama za mradi kwa usanifu wa awali zilikuwa kubwa zaidi. Kutokana na ongezeko la watu kutoka 12,019 mwaka 2007 hadi 17,686 kwa sasa mradi huo haukidhi mahitaji. Ili kukidhi mahitaji Serikali inakamilisha usanifu wa mradi utakaotoa maji Mto Misi ambapo ujenzi unatarajiwa kuanza mwaka 2018/2019.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba mradi wa maji Bulongwa na Magoma unaohudumia vijiji 14 uliojengwa mwaka 1984 haukukidhi mahitaji ya sasa na miundombinu yake ni chakavu. Serikali imeanza ukarabati wa mradi ambapo hadi sasa bomba jipya kwa umbali wa kilometa nne limelazwa na linahudumia Vijiji vya Unyangogo, Iniho na Mwakauta. Mchakato wa kumpata mkandarasi atakayetekeleza awamu ya pili ya ukarabati huo unaendelea ili kukarabati bomba kwa umbali wa kilometa mbili. Ukarabati wa mradi mzima unatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 30, 2018.
MHE. GODFREY W. MGIMWA (K. n. y. MHE. SUZANA C. MGONOKULIMA) aliuliza:-
Tangu kutangazwa sheria ya kuzitaka Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya wanawake na vijana.
Je, ni nini kinaifanya Serikali kutokuwa na taarifa ya mfuko huo kujua una kiasi gani cha fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suzana Chogisasi Mgonokulima, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, chimbuko la maelekezo yanayozitaka Halmashauri zote nchini kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo ya wanawake asilimia tano na mikopo ya vijana asilimia tano ni Azimio la Bunge la Agosti 1993, chini ya kifungu cha 17(1) cha Sheria ya Exchequer and Audit Ordinance ya mwaka 1961; likiazimia kuanzishwa kwa Mifuko Maalum ya Mikopo kwa Vijana na Wanawake kwa kuchangiwa asilimia 10 ya mapato ya ndani ya kila halmashauri kila mwaka. Baada ya azimio hilo Serikali ilitoa maelekezo mahsusi kwa Halmashauri zote nchini kutenga fedha hizo kuanzia mwaka wa fedha 1993/1994.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kadhaa za kiutekelezaji ambazo zimekuwa zikisababisha utekelezaji wa azimio hilo usifikie asilimia 100. Miongoni mwa changamoto hizo ni kutofikia viwango vya makusanyo ya ndani vilivyopangwa kwa mwaka husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mfano katika mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi 665,414,828,000 za mapato ya ndani zilipangwa kukusanywa na Halmashauri zote nchini; lakini mapato halisi yaliyokusanywa ilipofika mwisho wa mwaka yalikuwa ni shilingi 544,897,803,696 tu. Kutokana na ukusanyaji kutotabirika na hivyo kutofikia viwango tarajiwa, badala ya kiasi cha shilingi bilioni 56.8 kukopeshwa wanawake na vijana kama ilivyokuwa imetengwa, ni shilingi 17.5 tu sawa na asilimia 31, ndizo zilizotolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwakumbusha wakurugenzi wa halmashauri zote 185 Tanzania Bara kwamba kutotoa asilimia 10 ya mapato ya ndani ni tabia ambayo husababisha waandikiwe deni kwenye taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kupitia Bunge lako Tukufu, naagiza kuanzia sasa ni lazima kila Halmashauri itoe asilimia 10 ya mapato halisi ya ndani kama ilivyoelekezwa na Serikali ili kutokusababisha madeni ya aina hiyo.
MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-
Takwimu zinaonesha upungufu mkubwa wa matundu ya vyoo zaidi ya 200,000 katika shule mbalimbali za sekondari na msingi.
(a) Je, nini mkakati wa Serikali wa kumaliza tatizo hilo?
(b) Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kuja na mkakati mbadala kama ilivyofanya wakati wa kumaliza tatizo la madawati na maabara nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tuna upungufu wa matundu ya vyoo 276,198 kwa shule za msingi na 20,534 kwa shule za sekondari. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya matundu ya vyoo 6,708 kwa shule za msingi na 2,071 kwa shule za sekondari yamejengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya tathmini ya kina tumebaini kuwa zinahitajika jumla ya shilingi bilioni 646.822 kumaliza tatizo hilo. Wizara yangu imetoa maelekezo kwa halmashauri zote kwamba katika Bajeti ya mwaka 2018/2019, fedha za ruzuku ya maendeleo ambazo ni jumla ya shilingi bilioni 55.2 endapo zitapitishwa na Bunge, sehemu kubwa ya fedha hizo ielekezwe kwenye kipaumbele cha miundombinu ya elimu ikiwemo vyoo kwenye shule zote ambazo tayari wananchi watakuwa wamechangia nguvu zao.
Uamuzi huo utatoa nyongeza kubwa sana kwenye Bajeti ya shilingi bilioni 19.97 ambayo imetengwa chini ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mahsusi kwa ajili ya matundu ya vyoo katika shule za msingi na shule za sekondari. Mkakati wa Serikali ni kutumia fedha hizo kumalizia kazi za ujenzi ambazo zitakuwa zimeanzishwa na wananchi.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA aliuliza:-
Idadi ya watu nchini inazidi kuongezeka, ongezeko hili linaenda sambamba na ongezeko la mahitaji ikiwemo ardhi kwa ajili ya kilimo na ufugaji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea uwezo wakulima na wafugaji ili waendeshe shughuli zao katika maeneo madogo lakini kwa tija kubwa na kuwaondolea adha wanazozipata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Madaba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali huwajengea uwezo wakulima na wafugaji nchini kupitia elimu na ushauri wa kitaalam ambao hutolewa na Maafisa Ugani walioko kwenye Kata na Vijiji vya Halmashauri zote nchini. Hadi Desemba, 2017 tunao Maafisa Ugani 13,532. Kati ya hao Maafisa Ugani 8,232 ni wa kilimo cha mazao, 4,283 ni wa mifugo, 493 ni wa uvuvi na 524 ni wa ushirika.
Elimu ya kilimo na ufugaji bora hutolewa kupitia mashamba darasa 11,213 nchi nzima kwa wakulima na wafugaji wakubwa na wadogo, vikundi vya ushirika vya miradi ya umwagiliaji kwa njia ya mitaro na njia ya matone (drip irrigation) na vikundi vya ushirika vya ufugaji wa kisasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia awamu ya pili ya Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo itakayoanza kutekelezwa mwaka ujao 2018/2019 Serikali inaandaa mradi wa kilimo cha kutumia vitalu nyumba (green house) utakaotekelezwa kwa kila halmashauri kujenga vitalu nyumba visivyopungua viwili ili kusambaza teknolojia mpya ya kilimo yenye uwezo mkubwa wa kuzalisha shehena ya mazao mengi katika eneo dogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati mingine ni pamoja na kufanya sensa mahsusi ya kuwatambua wakulima wadogo na wakubwa, kuwasajili, kujua uwezo wao na kujua mahitaji yao ya mbegu, mbolea na madawa. Zoezi hilo limeanza na mazao ya kahawa, tumbaku, korosho, chai na pamba kwa mazao ya biashara; pamoja na mazao ya mahindi, mpunga, ngano na muhogo kwa upande wa mazao ya chakula. Takwimu hizo zitasaidia utekelezaji wa mikakati ya kuongeza uzalishaji kwa kuhakikisha pembejeo za kilimo zinawafikia wakulima mapema ili zitumike kwa wakati stahiki wa kilimo kwa lengo la kuongeza tija.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-
Kuna uhaba wa nyumba za kuishi walimu licha ya juhudi za wananchi kujenga nyumba za walimu wa shule za msingi na sekondari; walimu hao pia wanahitaji kujenga nyumba zao wenyewe za kudumu.
Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu wa kutoa mikopo kwa walimu ili wajenge nyumba zao binafsi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa upo uhaba wa nyumba za walimu katika shule za msingi na sekondari ndiyo maana imekuwa ikijitahidi kila mwaka kujenga nyumba za walimu. Katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 Serikali kwa kushirikiana na wananchi, imekamilisha ujenzi wa nyumba 274 za walimu na hivyo kufikisha idadi ya nyumba 14,640 kati ya nyumba 67,711 zinazohitajika kwenye shule za sekondari. Aidha, nyumba 290 za walimu zimejengwa kwenye shule za msingi na hivyo kufikisha idadi ya nyumba 45,638 kati ya nyumba 175,930 zinazohitajika. Takwimu hizo zinabainisha kwamba familia za walimu 52,071 katika shule za sekondari na familia za walimu 130,300 kwenye shule za msingi zinaishi kwenye nyumba za kupanga au nyumba zao binafsi. Ni wazi kwamba mahitaji ya nyumba za walimu ni makubwa mno.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imedhamiria kuendelea kuweka kipaumbele cha kujenga nyumba za walimu za kuishi familia mbili, nne au sita ambazo ni za gharama nafuu kulinganisha na gharama za kujenga nyumba za kuishi familia moja. Kipaumbele cha juu kitaendelea kuwekwa kwenye maeneo yenye mazingira magumu ya kupata nyumba za kupanga hasa maeneo ya vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa mikopo kwa ajili ya Walimu kujenga nyumba zao binafsi ni kama ulivyo kwa watumishi wengine wa Serikali, ambapo mtumishi anaruhusiwa kukopa kwenye taasisi au benki yenye mkataba maalum na mwajiri kwa kujaza fomu ili akatwe marejesho ya mkopo kutoka kwenye mshahara ambapo makato ya mkopo hayatakiwi kuzidi theluthi mbili ya mshahara na mkopo wote kulipwa kwa kipindi cha kati ya miezi 36 (miaka mitatu) hadi miezi 300 (miaka 25) kulingana na masharti ya taasisi husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa taasisi zinazotoa mikopo ya nyumba kwa watumishi wa Serikali wakiwemo walimu ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Kampuni ya Nyumba za Watumishi (Watumishi Housing Company), Benki ya Afrika (Bank of Africa – BOA) kupitia mpango wake wa WEZESHA, mabenki kadhaa mengine kama NMB, CRDB, Azania na kadhalika na kampuni nyingine kama vile T-Mortgage yanayolenga zaidi kuwakopesha watumishi wa kipato cha chini na cha kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili watumishi wakiwemo walimu wapate mikopo ya kujenga nyumba binafsi kwenye maeneo watakayochagua wao, inatakiwa Wakurugenzi wa Halmashauri wawasiliane na taasisi zinazokopesha ili waingie makubaliano maalum yatakayowawezesha watumishi wa Halmashauri wanaotaka mikopo ya kujenga nyumba binafsi wakiwemo walimu kupata mkopo.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza:-
Bwawa la Lukuledi ambalo huhudumia Kata za Lukuledi, Mpanyani na Chikinja ni muhimu sana kwa wananchi.
Je, Serikali itafanya lini ukarabati wa bwawa hilo kwa sababu kiwango cha maji kinapungua kwa kujaa mchanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Jimbo la Ndanda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali kupitia Wakala wa Uchimbaji Visima na Mabwawa (DDCA) inaendelea na kazi ya usanifu wa kina wa miundombinu ya Bwawa la Lukuledi lililojengwa mwaka 1954 ambalo ukarabati wake utakapokamilika litahudumia wananchi wapatao 11,544 kwenye vijiji vya Lukuledi A, Lukuledi B, Mraushi, Mkolopola, Ndomoni na Naipanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, usanifu huo unahusisha mabwawa mengine mawili yenye uwezo wa kuhudumia wananchi 15,746. Mabwawa hayo ni Bwawa la Mihima litakalohudumia vijiji vya Mihima, Muungano na Mpanyani na Bwawa la Chingulungulu litakalohudumia vijiji vya Chingulungulu, Namatutwe na Namalembo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la usanifu huo ni kubaini gharama zitakazohitajika kukarabati mabwawa hayo matatu yenye uwezo wa kuzalisha na kusambaza huduma ya maji kwa wananchi wapatao 27,290.
MHE. HAMIDU H. BOBALI aliuliza:-
Je, Serikali imefanya tathmini juu ya ubora na changamoto zilizopo katika shule za sekondari za kata nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la kitafiti la Mheshimiwa Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka 1995 hadi 2005 ni kipindi ambacho tafiti, tathmini, mikakati na mipango mingi katika sekta ya elimu, ikiwemo Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu (ESDP) inayotekelezwa kupitia Mpango wa Elimu ya Msingi (MMEM) kuanzia mwaka 2000 na Mpango wa Maendeleo wa Elimu ya Sekondari (MMES) kuanzia mwaka 2004 ilianzishwa.
Mipango hiyo ndiyo chimbuko la maamuzi ya kuanzisha Shule ya Sekondari kila Kata ili kuhakikisha watoto wengi zaidi waliokuwa wanakosa nafasi za masomo ya sekondari, licha ya kufaulu mitihani ya darasa la saba kwa sababu tu ya uchache wa shule wanapata nafasi hizo. Hadi mwezi Oktoba, 2017 tulikuwa na shule za sekondari za kata 3,103 zilizokuwa na wanafunzi 197,663 ambapo kama zisingekuwepo wangeikosa elimu ya sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini mbili za Serikali zilizochambua kwa kina sekta ya elimu kupitia Tume ya Profesa Mchome ya mwaka 2013 iliyochambua sababu za ufaulu hafifu wa wanafunzi kwenye mitihani ya mwaka 2012 ya kidato cha nne na Kamati kuhuisha na kuoanisha Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 1995, Sera ya Elimu ya Ufundi na Mafunzo mwaka 1996, Sera ya Taifa ya Elimu ya Juu ya mwaka 1999 na Sera ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa Elimu ya Msingi mwaka 2007 iliyoongozwa na Mwalimu Abubakar Rajab mwaka 2013, ndizo zilizobaini na kuishauri Serikali kuanzisha sera mpya moja ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014.
Mheshimiwa Naibu Spika, sera mpya imetoa maelekezo mahususi kuhusu namna ya kuboresha elimu ya awali, elimu ya msingi, elimu ya sekondari, elimu ya ufundi na elimu ya juu. Mitaala imesharekebishwa, ikama, vifaa, samani na miundombinu vyote hivi vinaendelea kuboreshwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa shule mpya, ujenzi wa madarasa, vyoo, maabara, mabweni, maktaba, nyumba za walimu, ofisi ya walimu, mabwalo na majengo ya utawala unaoendelea nchi nzima kwa kushirikiana na wananchi; kuboresha upatikanaji wa vitabu vya kiada na ziada katika shule za sekondari pamoja na juhudi za Serikali kuhakikisha walimu wa kutosha wanapatikana hasa wa masomo ya sayansi na hisabati, ni uthibitisho wa namna Serikali ilivyo na dhamira ya kuinua ubora wa elimu.
MHE. SALMA R. KIKWETE aliuliza:-
(a) Kwa kuwa elimu ni haki ya kila mtoto, je, Serikali inawasaidiaje watoto wenye usonji ili nao wapate elimu?
(b) Je, Walimu wanaofundisha watoto hao wanatosheleza kwa mujibu wa ikama?
(c) Kwa kuwa watoto hao wana mazingira tete, je, Walimu wao wana utaalam wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete, Mbunge wa Kuteuliwa, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, usonji ni ulemavu ambao huathiri mfumo wa mawasiliano katika ubongo, mahusiano na utambuzi. Wanafunzi wenye usonji wamekuwa wakifundishwa na Walimu watalaam wa ulemavu wa akili waliopatiwa mafunzo kazini. Hadi sasa tuna wanafunzi 1,416 wenye usonji na Walimu 157 walio katika shule 18 za msingi nchini. Walimu hao ni wachache na hawatoshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wapo Walimu waliopata taaluma hiyo kwenye Chuo cha Patandi, lakini hawako kwenye shule maalum, nasisitiza tena agizo langu nililolitoa kwenye Mkutano wa Kumi kwamba Halmashauri zote ziwahamishie Walimu hao kwenye shule zenye wanafunzi wenye ulemavu ikiwemo wenye usonji ifikapo mwezi wa Desemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa elimu maalum nchini kwa wanafunzi wenye ulemavu wasioona, viziwi, albino, usonji, viziwi–wasioona, walemavu wa akili, walemavu wa viungo, uoni hafifu, wenye vipawa na vipaji pekee pamoja na wenye matatizo ya ujifunzaji utaendelea kupewa kipaumbele. Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia ikiwemo miundombinu, vifaa maalum kwa mahitaji maalum, kutoa mafunzo zaidi kwa Walimu pamoja na kugharamia kwa ujumla elimu msingi bila malipo kwa wanafunzi wote ikiwemo wenye mahitaji maalum.
MHE. PAULINE P. GEKUL aliuliza:-
Kata ya Sigino na Vijiji vyake vyote katika Jimbo la Babati Mjini haina kabisa maji safi na salama:-
Je, ni nini mkakati wa Serikali wa kuipatia maji safi na salama Kata hiyo pamoja na Vijiji vyake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philip Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba vijiji vyote vinne katika Kata ya Sigino ndani ya Halmashauri ya Mji wa Babati vyenye wakazi 11,895 havina huduma ya maji safi na salama. Hata hivyo ziko hatua mahsusi zinazoendele. Mnamo tarehe 29 Mei, 2017, Halmashauri ya Mji wa Babati ilisaini mkataba wa Sh.487,470,000 kujenga mradi wa maji katika Kijiji cha Imbilili ambao ulipangwa kukamilika tarehe 30 Juni, 2018 lakini Mkandarasi Black Lion Limited amebainika kuwa na uwezo mdogo kwani hadi sasa ametekeleza kazi kwa asilimia saba tu. Naishauri Halmashauri ambapo Mheshimiwa Pauline Gekul ni Diwani, itathmini haraka hali hiyo na ichukue hatua haraka kwa manufaa ya wananchi.
Mheshimiwa Spika, hatua nyingine kubwa inayoendela ni utekelezaji wa mkataba kati ya Halmashauri na Mkandarasi Maswi Drilling Company Limited kuchimba visima virefu katika Vijiji vya Sigino, Singu na Haraa kwa shilingi milioni 94.5 ambao umefikia asilimia 25 na utakamilika tarehe 30 Juni, 2018. Usanifu na ulazaji wa mabomba yakayosambaza huduma za maji safi na salama kwa wananchi utaanza mwaka 2018/2019 kwa kutumia Sh.611,137,000 ambazo zimetengwa kutekeleza mradi huo. Ahsante.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA aliuliza:-
Kiwango cha elimu katika Mkoa wa Tabora kimeshuka sana, Mkoa umefanya vibaya katika mtihani wa darasa la saba, kidato cha nne na cha sita. Kufanya vibaya kunatokana na changamoto mbalimbali kama walimu, upungufu wa madawati na idadi kubwa ya wanafunzi katika madarasa.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kero hizi zinatatuliwa ili kurejesha hadhi ya elimu Mkoa wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, ambaye ni mtoto wa shangazi yangu na Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto zilizotajwa katika swali, si kweli kwamba kiwango cha elimu kimeshuka sana Mkoani Tabora kwa kufanya vibaya kwenye mitihani. Takwimu zinathibitisha hali tofauti kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, katika mitihani ya darasa la saba ya mwaa 2016 kiwango cha ufaulu kilikuwa asilimia 71.35 ambapo Mkoa wa Tabora ulishika nafasi ya 10 kitaifa, lakini mwaka 2017 ufaulu ulipanda hadi asilimia 73.61 na Mkoa ukaendelea kushika nafasi ya 10 kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, katika mitihani ya kidato cha nne ya mwaka 2016 kiwango cha ufaulu kilikuwa asilimia 71 ambapo Mkoa wa Tabora ulishika nafasi ya 10 kitaifa, lakini mwaka 2017 ufaulu ulipanda hadi asilimia 84 na Mkoa kushika nafasi ya 3 Kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kwa upande wa kidato cha sita, ufaulu mwaka 2016 ulikuwa asilimia 97.8 na Mkoa wa Tabora ulishika nafasi ya 11 kitaifa. Kwa mwaka 2017 pamoja na takwimu kuonesha kuwa ufaulu ulikuwa asilimia 87, nafasi ya mkoa kitaifa ilipanda hadi nafasi ya 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka yote miwili mfululizo, Mkoa wa Tabora umekuwa juu ya wastani wa ufaulu kitaifa, hilo ni jambo la kujivunia. Kwa hali hiyo hatuwezei kusema kiwango cha elimu katika Mkoa wa Tabora kimeshuka bali kimepanda. Serikali ina kila sababu ya kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mheshimiwa Aggrey Mwanri na viongozi wote wa Mkoa wa Tabora wakiwemo viongozi wa wilaya zote na hamashauri zote kwa juhudi zao zilizowezesha matokeo hayo mazuri.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-
Ubora wa elimu wanayopata watoto wa jamii ya kifugaji wanaosoma shule za kutwa vijijini unaathiriwa sana na umbali mrefu wanaotembea wanafunzi kutoka makazi yao (maboma) hadi shuleni.
(a) Je, ni kwa nini Serikali isijenge mabweni katika baadhi ya shule zilizo kwenye vijiji vyenye mtawanyiko mkubwa wa maboma?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi wa Longido kujenga vyumba 177 vya madarasa, nyumba 291 za walimu na matundu 561 ya vyoo?
(c) Je, Serikali imepanga lini kuziba upungufu wa walimu 234; Waratibu Elimu Kata 18 na maafisa ngazi ya Wilaya 12 katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali refu la Mheshimiwa Dkt. Steven Lemomo Kiruswa, Mbunge wa Longido, lenye vipengele (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto inayowakabili watoto wa jamii ya kifugaji ndivyo maana katika kipindi cha kuanzia Julai, 2017 hadi Aprili, 2018 imekamilisha ujenzi wa bweni la wasichana na matundu 14 ya vyoo na inaendelea na ujenzi wa bweni la wavulana na nyumba tatu za Walimu katika Shule ya Msingi Sinya.
Vilevile nyumba ya Walimu two in one na madarasa matatu yanaendelea kujengwa katika Shule ya Msingi Kitumbeine ambao yatakamilika Juni, 2018.
Aidha, katika Shule ya Msingi Longido, ujenzi wa vyumba nne vya madarasa uko katika hatua ya msingi. Shule hizo tatu zina uwezo wa kuhudumia wanafunzi 1,323. Utekelezaji huo unafanyika ili kuwapunguzia adha watoto wa jamii ya kifugaji ambao kwa wastani hutembea zaidi ya kilometa 15 kutoka nyumbani hadi shuleni.
Aidha, ujenzi wa madarasa 24 kwenye Shule za Ranch, Imatiani Sokoni, Olmoti, Olmolog na Engurusai vimekamilika wakati ujenzi wa madarasa 18 katika shule mbalimbali unaendelea. Ujenzi wa bweni katika Shule ya Msingi Ngerenyai umekamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 515. Kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo, vyumba vya madarasa na nyumba za walimu. Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi na wadau itaendelea kujenga mabweni kwenye maeneo ya wafugaji na maeneo mengine yenye uhitaji kadri ya upatikanaji wa fedha utakavyowezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Longido ina Kata 18 ambazo kwa sasa Kata zote zina Maafisa Elimu Kata. Katika ngazi ya Halmashauri ya Wilaya kuna upungufu wa Afisa Elimu vielelezo baada ya aliyekuwepo kuhamishwa kwenda Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC). Serikali itaziba pengo hilo hivi karibuni, sambasamba na kupunguza upungufu wa walimu katika Shule za Msingi na Sekondari.
MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y MHE. JOHN W. HECHE) aliuliza:-
Mazingira ya ufundishaji kwa Walimu walio wengi nchini ikiwemo Wilaya ya Tarime yamekuwa siyo rafiki, ambapo Walimu wamekuwa wakibebeshwa mzigo wa gharama za vifaa vya kufundishia kama maandalio ya somo, chaki na kadhalika:-
Je, matumizi haya yatarekebishwaje katika mfumo huu wa elimu bure ulioanzishwa na Serikali ya Awamu ya Tano.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kwa ruhusa yako, nimpe pole Mheshimiwa John Heche na wote ambao wamefiwa, Serikali ipo pamoja nao katika misiba hiyo.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, ambapo marekebisho yake madogo naomba yaingie katika Hansard kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kupitia Waraka wa Elimu Na.5 wa mwaka 2015, uliotoa mwongozo wa Serikali kuhusu Elimu Msingi bila malipo, majukumu ya Serikali, jamii, wazazi, walezi, wakuu wa shule, Kamati au Bodi za shule, yamefafanuliwa vizuri sana kwenye Waraka huo. Miongoni mwa majukumu ya Serikali ni kutoa ruzuku ya uendeshaji wa shule, inayogharamia chakula kwa wanafunzi wa bweni, ununuzi wa vitabu vya kiada na ziada, vitambulisho, mitihani endelezi, mitihani ya Taifa, shughuli za michezo, maandalio ya somo, chaki na vifaa vingine. Hivyo siyo sahihi kwa Walimu kutumia fedha zao kugharamia maandalio ya somo na vifaa kama chaki.
Mheshimiwa Spika, nawaagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri, Maafisa Elimu wote wa ngazi zote na Walimu Wakuu kusimamia vizuri Mpango wa Utoaji Elimu Msingi bila malipo kama ulivyofafanuliwa katika waraka nilioutaja, kuanzia sasa Walimu wasikubali kubebeshwa mizigo ya gharama isiyowahusu.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya mipaka ya baadhi ya maeneo kama vile mikoa, wilaya na majimbo ya uchaguzi kwani baadhi ya mipaka ya maeneo hayo yana muingiliano unaoleta ugumu wa utoaji wa huduma za jamii?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuligawa Jimbo la Mbinga Vijijini kwa kuzingatia ukubwa wake wa kata 29?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kufanya mapitio ya mipaka kwa baadhi ya mikoa, wilaya na majimbo ya uchaguzi hasa yenye muingiliano unaosababisha ugumu wa utoaji wa huduma za jamii. Hata hivyo, zoezi hilo ambalo linaweza kusababisha mapendekezo ya maeneo mapya ya utawala au kuyahamisha mengine litafanyika baada ya kukamilisha miundombinu ya majengo ya ofisi, majengo ya huduma mbalimbali na vifaa katika mikoa, wilaya na halmashauri mpya zilizoanzishwa tangu mwaka 2012.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imepewa mamlaka ya kuyagawa majimbo ya uchaguzi kwa kuzingatia vigezo vya idadi ya watu, jiografia, hali ya mawasiliano, ukubwa wa jimbo na uwezo wa ukumbi wa Bunge. Ili jimbo ligawanywe Tume hutoa tangazo kuhusu nia hiyo. Baada ya tangazo, mapendekezo hujadiliwa katika vikao vya halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa na hatimaye huwasilishwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo hutangaza Jimbo jipya baada ya kupata kibali cha Rais.
MHE. ALMAS A. MAIGE aliuliza:-
Halmashauri ya Wilaya ya Uyui inajulikana kwa jina la zamani la Tabora District Council (TDC) jina ambalo linagongana na jina la Manispaa ya Tabora (Tabora Minicipality). Wilaya kupitia Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa alileta maombi ya kubadili jina la Halmashauri kutoka Tabora District Council (TDC) na kuwa Halmashauri ya Uyui na Halmashauri imeomba kubadili jina la Jimbo la Tabora Kaskazini na Jimbo la uyui ikibeba jina la Wilaya na jina la eneo la kijiografia Uyui kwa sababu, hakuna tena Tabora Kaskazini, Kusini wala Magharibi:-
(a) Je, ni lini jina la Halmashauri litabadilishwa kuwa Halmashauri ya Uyui?
(b) Je, ni lini Jimbo la Tabora Kaskazini litaitwa Jimbo la Uyui?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Maige, naomba kwanza dakika moja tu nielezee furaha yangu; leo nimeamka saa 10:00 usiku kwa ajili ya kujiandaa kuja kujibu maswali, lakini furaha yangu kubwa ni kwa sababu Simba Sports Club baada ya kupata ubingwa sasa naamini Watanzania watapata wawakilishi kwenye michezo ya kimataifa ambao hawatatupa pressure kwa sababu vijana hawa wanajua kucheza vizuri sana mpira wa miguu, ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya maelezo hayo…
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge a Tabora Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mhesimiwa Mwenyekiti, maombi yenye mapendekezo ya kubadili jina la Halmashauri ya Wilaya ya Tabora kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Uyui sawa sawa na jina la Wilaya ya Uyui ambayo yamepitishwa na vikao vya kisheria vya Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Kamati ya Ushauri ya Mkoa yameshapokelewa na yako katika hatua za kupata ridhaa. Nawaomba wadau wote wa suala hili wawe na subira wakati Serikali inapomalizia mchakato huo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mapendekezo ya kubadili jina la jimbo yaliyoridhiwa na baraza, wilaya na mkoa yanatakiwa kuwasilishwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo ndio yenye mamlaka ya uamuzi. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA aliuliza:-
Mwaka wa 2014/2015, Jimbo la Magu halikupatiwa Walimu wa shule za msingi na bado kuna uhaba wa Walimu:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta Walimu Magu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniventura Desderius Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Magu inao Walimu wa shule za msingi 1,281 kati ya Walimu 2,002 wanaohitajika, hivyo kuna upungufu wa Walimu 821. Kati ya Walimu 1,276 wa shule za msingi walioajiriwa mwezi Disemba, 2017, Halmashauri ya Wilaya ya Magu ilipangiwa Walimu 56 ambao wameripoti kwenye shule zilizokuwa na uhitaji mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Walimu 77 ambao ni miongoni mwa Walimu wa ziada wa masomo ya sanaa katika shule za sekondari za Halmashauri ya Wilaya ya Magu wamehamishiwa shule za msingi. Vile vile katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, Serikali imepanga kuajiri Walimu 10,130 wa shule za msingi nchi nzima ili kukabiliana na uhaba wa Walimu katika maeneo mbalimbali; na Halmashauri ya Magu nayo itapangiwa Walimu hao. (Makofi)
MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-
Jimbo la Mpwapwa lina tarafa mbili, yaani Tarafa ya Mpwapwa na Tarafa ya Mima, lakini tangu kuanzishwa kwa Tarafa ya Mima hakuna miundombinu yoyote iliyojengwa kama vile Ofisi ya Tarafa na vyumba vya watumishi:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Ofisi ya Afisa Tarafa na za watendaji wengine wa ngazi ya tarafa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Afisa Tarafa wa Tarafa ya Mima hajajengewa ofisi, anatumia Ofisi ya Afisa Mtendaji wa Kata ya Mima kutekeleza majukumu yake. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga Sh.50,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Afisa Tarafa huyo itakayojengwa katika Kijiji cha Mima.
MHE. COSATO D. CHUMI (K.n.y. SAUL H. AMON) aliuliza:-
Jimbo la Rungwe ambalo lina kata 29 lina vituo viwili tu vya afya ambavyo ni Masukulu na Ikati; wananchi wa Kata ya Mpuguso na Isongole kwa nguvu zao wameanzisha ujenzi wa vituo vya afya:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia kumaliza ujenzi huo ili kuwapunguzia adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu katika Hospitali ya Wilaya ambayo baadhi ya maeneo ni takriban kilometa 50 na usafiri usio wa uhakika?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saul Henry Amon, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na uboreshaji wa vituo vya afya 208 nchi nzima ili kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa wagonjwa karibu na wanapoishi. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Serikali imetoa jumla ya shilingi bilioni 1, yaani mwezi Septemba, 2017 ilipeleka Sh.500,000,000 kwenye Kituo cha Afya cha Ikuti kwa ajili ya kujenga jengo la wagonjwa wa nje (OPD), chumba cha upasuaji, wodi ya watoto, wodi ya akina mama wajawazito, jengo la kuhifadhia maiti, jengo la kufulia la kisasa, mtambo wa oxygen na kukarabati miundombinu ili kuhakikisha huduma za upasuaji wa dharura kwa mama wajawazito na huduma nyingine zinapatikana katika Kata ya Ikuti badala ya kufuata huduma hizo kwenye hospitali ya wilaya ambayo iko mbali. Aidha, mwezi Aprili, 2018 Serikali imepeleka Sh.500,000,000 kwenye Kituo cha Afya cha Masukulu ili kujenga na kukarabati miundombinu itakayoboresha huduma kama ilivyo kwa Kituo cha Afya cha Ikuti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, Kituo cha Afya cha Mpuguso kimetengewa shilingi milioni 100 kutoka kwenye mapato ya ndani ya halmashauri kwa ajili ya kumalizia jengo la wagonjwa wa nje (OPD). Sambamba na kuitaka halmashauri itenge fedha za mapato ya ndani ili kuendeleza ujenzi kwenye Kituo cha Afya cha Mpuguso na kuanza ujenzi kwenye Kituo cha Afya cha Isongole, napenda kutoa ahadi kwamba Serikali itavipa vituo hivyo kipaumbele cha juu ili ikiwezekana vikamilike mwakani.
MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:-
Watendaji wa Vijiji ni kada muhimu sana katika kuwahudumia wananchi walio vijijini:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia mafunzo ya mara kwa mara watumishi hawa ili kuboresha utumishi wao na utoaji huduma kwa wananchi walioko vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edward Franz Mwalongo, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watendaji wa Vijiji kama walivyo watumishi wengine wa umma wanapaswa kupewa mafunzo mara kwa mara ili kuboresha utendaji na kuongeza ufanisi. Mafunzo yanayotolewa kwa Watendaji wa Vijiji hujumuisha masuala ya utawala bora, mapambano dhidi ya rushwa, mapambano dhidi ya UKIMWI mahali pa kazi, maadili ya utumishi wa umma pamoja na majukumu yao katika utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia ruzuku ya maendeleo kwa Serikali za Mitaa ambayo inajumuisha Mpango wa Mafunzo kwa watumishi wa kada mbalimbali, Watendaji wa Vijiji 1,840 walipewa mafunzo katika mwaka wa fedha 2016/17. Kuanzia Julai 2017 hadi Aprili 2018 kwa mwaka huu unaoendelea, Watendaji wa Vijiji 1,543 wamepewa mafunzo. Mpango huu ni endelevu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kuziagiza halmashauri zote nchini kuweka kipaumbele na kutenga bajeti ya mafunzo kwa kada hii muhimu na kuanzia mwakani tutaanza kufuatilia utekelezaji wa agizo hili ili kuhakikisha kuwa limezingatiwa na halmashauri zote wakati wa bajeti.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-
Wabunge wa Viti Maalum ni sawa na Wabunge wengine wa Majimbo kwa sababu hakuna tofauti ya kiapo cha Wabunge wa Majimbo na wale wa Viti Maalum.
Je, ni kwa nini Wabunge wa Viti Maalum hawaingii kwenye Vikao vya Kamati ya Fedha za Halmashauri zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango, imeundwa kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287, kifungu cha 75 na Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji), Sura ya 288 kifungu cha 47 pamoja na kifungu cha 40(2)(c) cha Kanuni za Kudumu za Halmashauri za mwaka 2014 na Kanuni za Kudumu za Mamlaka za Serikali za Mitaa kifungu 41(1) zinazotaja Wajumbe wa kuingia kwenye Kamati ya Fedha na Mipango kuwa ni Meya au Mwenyekiti wa Halmashauri ambaye atakuwa Mwenyekiti; Naibu Meya au Makamu Mwenyekiti, Mbunge au Wabunge wa Majimbo wanaowakilisha Majimbo katika Halmashauri hiyo; Wenyeviti wa Kamati za Kudumu katika Halmashauri; Wajumbe wengine wasiozidi wawili watakaopendekezwa na Mwenyekiti au Meya na kupigiwa kura na Baraza la Madiwani la Halmashauri, mmoja kati yao akiwa mwanamke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wa Viti Maalum hawaingii kwenye vikao vya Kamati za Fedha za Halmashauri kwa sababu hawajatajwa kwenye orodha ya Wajumbe iliyoainishwa na kifungu cha 41(1) na kifungu cha 40(2) cha Kanuni za Kudumu za Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mwaka 2014, zinazofafanua mahitaji ya Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287, kifungu cha 75 na Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura ya 288 kifungu cha 47.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza:-
Serikali imeanzisha Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC)
kwa lengo la kutatua matatizo ya walimu.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha Tume hiyo ili ifanye kazi kikamilifu kama ilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) imeanzishwa kwa Sheria ya Utumishi wa Walimu Namba 25 ya mwaka 2015 na kuanza kutekeleza majukumu yake rasmi tarehe 1Julai, 2016 kupitia Ofisi za Tume zilizopo katika Wilaya 139 za kiutawala ambazo zinasimamiwa na Makatibu Wasaidizi wa Wilaya. Majukumu ya tume yameainishwa katika kifungu cha 5 cha Sheria hiyo ambayo ni pamoja na kusimamia mikataba ya ajira za walimu, kuwapandisha madaraja na kuchukua hatua za kinidhamu, ikiwemo kusikiliza rufaa kutoka ngazi za chini, kuwatambua na kutunza kumbukumbu za walimu wa shule za msingi na sekondari, kusimamia mafunzo ya walimu walio kazini, kufanya tafiti mbalimbali zinazohusu utumishi wa walimu na kutathmini hali ya utumishi wa walimu na kusimamia maadili ya utumishi wa walimu.
Mheshimiwa Spika, huu ni mwaka wa pili tu wa uhai wa Tume hiyo ambayo bado ni changa. Mikakati mahususi ya Serikali ili kuiimarisha zaidi Tume hiyo ni ifuatayo:-
• Kuendelea kuipatia fedha ili iweze kutimiza majukumu yake ipasavyo. Mfano katika mwaka wa fedha 2018/2019 Bunge limeiidhinishia Tume ya Utumishi wa Walimu shilingi 12,515,260,520 kati ya hizo shilingi 7,893,115,025 ni za mshahara na shilingi 4,622,145,495 ni za matumizi mengineyo, ili Tume ipate vitendea kazi kama magari, samani za ofisi na pia kugharamia vikao vya mashauri ya nidhamu na vifaa.
• Kuipatia ofisi na watumishi wa kudumu, mfano, hadi sasa inao Makatibu Wasaidizi wa Wilaya 138 ambao wameshajengewa uwezo na mwaka ujao 2018/2019 wataajiriwa watumishi 45 wapya na wengine 145 watahamishiwa kwenye Tume kama uhamisho wa kawaida. Uimarishaji wa Tume hiyo utaendelea kufanyika ndani ya wigo wa sheria iliyoanzisha Tume hiyo.
MHE. NASSOR SULEIMAN OMARY aliuliza:-
Uhakiki wa vyeti feki umeathiri wafanyakazi wengi na wengine wamepoteza ajira zao:-
Je, ni wafanyakazi wangapi wamepoteza ajira zao sekta ya elimu pekee?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Suleiman Omar, Mbunge wa Ziwani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 na 2017/2018, Serikali ilifanya uhakiki wa vyeti vya watumishi wa umma ili kubaini waliokuwa na vyeti halali na waliokuwa na vyeti vya kughushi. Katika uhakiki huo, jumla ya Walimu 3,655 walibainika kuwa na vyeti vya kughushi, hivyo walipoteza sifa za kuendelea kuwa watumishi wa umma.
MHE. OMARI A. KIGODA aliuliza:-
Je, ni kwa kiasi gani Serikali inasimamia suala la asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwa ajili ya vijana na akina mama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omari Abdallah Kigoda, Mbunge wa Handeni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhakikisha halmashauri zote nchini zinatenga asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Katika Mwaka wa Fedha 2016/2017, jumla ya shilingi bilioni 56.8 zilitengwa na halmashauri zote nchini na jumla ya shilingi bilioni 17.5 sawa na asilimia 31 zilitolewa kwa vikundi vya wanawake na vijana. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 jumla ya shilingi bilioni 61.6 zilitengwa na hadi kufikia Februari, 2018 jumla ya shilingi bilioni 15.6 sawa na asilimia 27 zilikuwa zimetolewa, ambapo jumla ya vikundi 8,672 vya wanawake na vijana vilipatiwa mikopo. Katika mwaka wa fedha 2018/ 2019, shilingi bilioni 53.8 zimetengwa kwa ajili ya Mfuko wa Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu katika halmashauri zote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza uwajibikaji katika kutenga na kupeleka fedha za Mfuko wa Wanawake na Vijana kwa vikundi husika, Serikali itaweka utaratibu katika Sheria ya Fedha (Finance Bill) ya mwaka 2018/2019 utakaohakikisha kwamba halmashauri zote zinatekeleza kikamilifu agizo hilo. (Makofi)
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH (K.n.y. MHE. HASSAN S.
KAUNJE) aliuliza:-
(a) Je, ni lini Serikali itadhamini Wenyeviti wa Serikali za Mitaa ili waweze kupata mikopo kama ilivyo kwa Madiwani na Wabunge?
(b) Je, ni lini Serikali itaanza kuwalipa posho/ mishahara Wenyeviti wa Serikali za Mitaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Kaunje, Mbunge wa Lindi Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, utaratibu wa Halmashauri na Bunge kudhamini mikopo kwa Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa Wabunge umetokana na kuwepo kwa utayari wa benki zinazokopesha mikopo hiyo, hususan NMB na CRDB ambazo baada ya kuonesha utayari, makubaliano maalum husainiwa ambayo ndiyo hutoa mwongozo wa namna mikopo itakavyotolewa pamoja na viwango vyake.
Mheshimiwa Spika, utaratibu wa aina hiyo hadi sasa haujawezekana kwa Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Mitaa na Vitongoji kwa kuwa hadi sasa hakuna benki iliyoonesha utayari wa kutoa mikopo ya aina hiyo. Hata hivyo, ipo fursa kwa kiongozi mmoja mmoja kuwasiliana na benki moja kwa moja kwa ajili ya makubaliano binafsi ya mkopo kulingana na kiwango cha amana alichonacho, thamani ya ardhi, nyumba anayomiliki au biashara.
(b) Mheshimiwa Spika, kwa kutambua kazi kubwa inayofanywa na Wenyeviti wa Serikali za Vijiji, Vitongoji na Mitaa kupitia Mpango wa Maboresho ya Serikali za Mitaa, Serikali ilitoa mwongozo kuwa viongozi hao wawe wanalipwa posho inayotokana na asilimia 20 ya mapato ya ndani ambayo hurejeshwa na Halmashauri kwenye Kijiji/Mtaa husika.
Mheshimiwa Spika, changamoto zilizopo za ukusanyaji hafifu wa mapato ya ndani zimekuwa zikisababisha ugumu wa kutekeleza mwongozo huo katika baadhi ya maeneo. Kwa sababu hiyo, Halmashauri zote zimeagizwa zifanye mapitio ya vyanzo vyote vya mapato na ziimarishe makusanyo ya ndani ili ziwe na uwezo wa kulipa posho hizo.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-
Kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu wa mpaka kati ya Wilaya ya Liwale na Wilaya ya Kilwa:-
Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro huo ili kuleta amani katika Wilaya hizo kabla amani haijatoweka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kilwa ilianzishwa kwa Tangazo la Serikali Na. 91 la tarehe 16 Mei, 1947 na Wilaya ya Liwale ilianzishwa kwa Tangazo la Serikali Na.185 la tarehe 5 Desemba, 1980. Hadi hapo hakukuwa na mgogoro wowote. Tangazo la Serikali Na. 134 la mwaka 1983 lilianzisha Halmashauri za Wilaya ambapo Mirui iliorodheshwa kama kata na kijiji katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale na haikutajwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa.
Mheshimiwa Spika, Serikali inautambua mgogoro huo unaohusu mkanganyiko ulioko kati ya Kitongoji cha Mirui katika Kijiji cha Nanjirinji A, Kata ya Nanjirinji, Wilayani Kilwa kwa upande mmoja na Kijiji cha Mirui katika Kata ya Mirui Wilayani Liwale kwa upande wa pili.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mgogoro huo ni sehemu ya migogoro mingi inayoshughulikiwa na Serikali chini ya uratibu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, nashauri Mbunge na wananchi wa maeneo husika wawe na subira wakati huu ambapo Serikali imetuma wataalam kwenye eneo hilo la mgogoro wanaofanya mapitio ya kina ya matangazo ya kuanzisha wilaya zote mbili na tangazo la kuanzisha halmashauri zote mbili kwa lengo la kuhakikisha mgogoro huo unapatiwa ufumbuzi wa kudumu ndani ya mwaka 2018/2019.
MHE. SONIA J. MAGOGO aliuliza:-
Je, Serikali inasaidiaje watoto wa Shule za Msingi Wilayani Handeni ambao wamekuwa wakisongamana sana kwenye darasa moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwanza naomba uniruhusu nimkaribishe Mheshimiwa Sonia kwenye kazi za Bunge baada ya kuwa ameugua kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sonia Jumaa Magogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ongezeko la wanafunzi katika shule za msingi na sekondari ni moja ya changamoto iliyotokana na utekelezaji wa Sera ya Elimu Bila Malipo. Katika mwaka wa fedha 2016/2017, Serikali ilikamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa sita kwa kiasi cha shilingi milioni 40.96 katika shule za msingi Kwazala, Ugweno na Gumba na Mbunge wa Handeni Mheshimiwa Mboni Mhita, kupitia fedha za Mfuko wa Jimbo alikamilisha ujenzi wa madarasa saba kwa gharama ya shilingi milioni 37.63 katika shule za Kabuku Mjini, Gole, Mnyuzi na Msilwa.
Mheshimiwa Spika, vilevile katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imejenga vyumba sita vya madarasa kwa gharama ya shilingi milioni 120 katika Shule za Mhalango, Kitumbi na Komkonga na kukamilisha ujenzi wa vyumba sita vya madarasa kwa gharama ya shilingi milioni 23.5 katika Shule za Kwachaga na Kibundu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 137.2 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba sita vya madarasa na matundu 12 ya vyoo katika Shule za Msingi Kiselya na Mhalango.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga miundombinu ya elimu katika Halmashauri ya Handeni na inawaomba wananchi na wadau kushiriki kikamilifu katika juhudi za kupunguza tatizo la uhaba wa vyumba vya madarasa, maana Serikali peke yake haitoweza kuwa na bajeti ya kutosheleza mahitaji yote ya Ujenzi wa miundombinu ya shule kwa kipindi kifupi.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-
Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ina jumla ya kata 39 na vijiji 157. Halmashauri iliomba kuigawa Wilaya hiyo ambayo ina ukubwa zaidi ya Mkoa wa Mtwara wenye Wilaya sita:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuigawa Wilaya ya Tunduru ili iwe rahisi kutoa huduma karibu zaidi na wananchi?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuzigawa Kata za Mchoteka, Mtina, Namasakala, Lukumbule, Mchasi, Tuwemacho na Misechela ambazo zina wakazi zaidi ya 30,000 kila Kata?
(c) Je, Serikali itaidhinisha lini mgao wa vijiji uliopendekezwa na Halmashauri mwaka 2015 ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, taratibu za kuanzisha au kugawanya maeneo ya kiutawala zimeainishwa kwenye Sheria ya Serikali za Mitaa Sura ya 287, pamoja na Mwongozo wa Serikali wa mwaka 2014.
Mheshimiwa Spika, maombi ya kugawa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru na kuanzisha Halmashauri ya Wilaya ya Nalasi na kuzigawa Kata za Mchoteka, Mtina, Namasakala, Lukumbule, Mchasi, Tuwemacho na Msecheke yaliwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI yakiwa pamoja na ombi la kuanzisha mkoa mpya wa Selous. Serikali imetafakari maombi haya na kuyaona kuwa ni ya msingi, hata hivyo, kutokana na changamoto ya kuimarisha kwanza miundombinu kama majengo ya ofisi na nyumba za watumishi na mahitaji mengine kama vifaa vya ofisi, watumishi wa kutosha na vyombo vya usafiri kwenye maeneo mapya ya utawala yaliyoanzishwa tangu mwaka 2010 na 2012, Serikali imesitisha uanzishwaji ya maeneo mapya ya utawala hadi yaliyopo yaimarishwe kikamilifu.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Katika Mji Mdogo wa Mbalizi kuna ardhi ya ukubwa wa zaidi ya ekari 5,000 iliyotengwa kwa ajili ya Tanganyika Packers ambayo haijaendelezwa kwa zaidi ya miaka 30 iliyopita.
(a) Je, ni lini Serikali itawarudishia wananchi wa Mji Mdogo wa Mbalizi eneo hilo kwa lengo la kuliendeleza kwa kubadili matumizi kutokana na kukua kwa kasi kubwa kwa Mji wa Mbalizi?
(b) Pamoja na kubadili matumizi ya ardhi hiyo, je, Serikali ina mpango gani kwa wananchi wanaotumia ardhi hiyo hasa ikizingatiwa kuwa wengi wao hawakupewa fidia yoyote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba namba 760 lenye hekta 102.4 na shamba namba 761 lenye hekta 1985.4 yaliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ambayo kwa pamoja yana ukubwa wa hekta 2,087.8 sawa na ekari 5,219.5 ni mali ya Serikali. Mwaka 1974 Serikali ilijenga Kiwanda cha Kusindika Nyama cha Tanganyika Packers kwenye shamba namba 760 na shamba namba 761 lilikuwa maalum kwa ajili ya kupumzisha mifugo na kuilisha vizuri kabla ya kuchinjwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya uzalishaji kiwandani kusimama kutokana na changamoto kadhaa za kiuendeshaji na kiuchumi, baadhi ya wananchi walivamia maeneo ya mashamba hayo na tarehe 4/3/2016, Halmashauri ya Wilaya iliomba kwa Msajili wa Hazina kubadilisha matumizi ya eneo hilo kuwa makazi na huduma nyingine. Ombi hilo lilikataliwa kwa kuwa nia ya Serikali kuliendeleza eneo hilo kama eneo la viwanda haijawahi kubadilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo maana ili kuona kuwa haki inatendeka Serikali ilifungua kesi Namba 1 ya mwaka 2015 Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya dhidi ya wavamizi ambayo ilihukumiwa tarehe 20/2/2018 kwa Serikali kupewa haki ya kuendeleza eneo lake. Taratibu za kisheria za kuwaondoa wavamizi ili eneo hilo litumike kama ilivyokusudiwa zitakamilishwa hivi karibuni. Serikali haijawahi na haina mpango wa kubadili matumizi ya eneo hilo, kwani kufanya hivyo kwa maeneo kama hayo ni kukwamisha juhudi za kujenga Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kumbukumbu zilizopo wananchi waliokuwa wanastahili fidia kwa mujibu wa sheria wote walilipwa.
MHE. KANALI MST. MASOUD ALI KHAMIS (K.n.y. MHE. IBRAHIM HASSANALI MOHAMMEDALI) aliuliza:-
Jiji la Dar es Salaam linakabiliwa na tatizo la ombaomba wengi na katika baadhi ya maeneo wamejenga miundombinu ya kulala.
Je, ni lini Serikali itachukua hatua ya kuwaondoa
ombaomba katika Jiji la Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ibrahim Mohamedali Raza, Mbunge wa Kiembesamaki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba wapo ombaomba katika baadhi ya maeneo ya Jiji la Dar-es-Salaam kwa sababu vipo vivutio vingi ikiwemo watu wenye imani mbalimbali ambao huwapatia fedha na vitu vingine kama sehemu ya ibada. Kuzagaa kwa ombaomba kimekuwa chanzo kimojawapo cha uchafuzi wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto za ombaomba mara kadhaa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar-es-Salaam imetekeleza hatua mbalimbali za kuwaondoa, ikiwemo kuwakamata na kuwasafirisha makwao, lakini wamekuwa wakirudi. Mfano mwezi Septemba, 2013 ombaomba 253 na watoto 135 walirejeshwa kwao ambapo watoto 33 walirejeshwa shuleni. Hii inathibitisha kuwa wapo watu wazima wanaotumia watoto kuombaomba. Watanzania wanatakiwa kuzitumia fursa za kupambana na umaskini zilizoandaliwa na Serikali, ikiwemo elimu msingi bila malipo, huduma za afya vijijini na uwepo wa Sheria ya Fedha 2018 inayotoa fursa kwa makundi mbalimbali ya uzalishaji mali kupata mikopo, wakiwemo walemavu. Vilevile watumie uwepo wa ardhi ya kutosha yenye rutuba kama fursa ya kuweza kujitegemea na hivyo, kujikomboa dhidi ya kuombaomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ombaomba wamekuwa wakisababisha watoto wengi kutopata fursa ya kusoma shule au kuwa watoro, nawaagiza Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri chini ya usimamizi wa Wakuu wa Mikoa kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama kuwakamata wototo wote ambao badala ya kwenda shuleni huzagaa mitaani wakiombaomba, wakamatwe pamoja na wazazi wao na washtakiwe Mahakamani chini ya Sheria ya Elimu ya mwaka 78 inayokataza utoro na Sheria ya Kanuni ya Adhabu Kifungu cha 166, 167 na 169A vinavyohusu wajibu wa wazazi na walezi kwa watoto. Aidha, Mabaraza ya Madiwani nayo yanaweza kutunga Sheria Ndogo za kuzuia utoro pamoja na kudhibiti mienendo ya baadhi ya watu kuombaomba.
MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-
Je, Serikali haioni haja sasa ya kuziagiza rasmi Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwezesha Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) kutekeleza baadhi ya majukumu yake ili walimu wapate huduma stahiki kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Singida Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Utumishi wa Walimu ilianzishwa kwa Sheria Na. 25 ya mwaka 2015 ili kuwahudumia walimu wa shule za msingi na sekondari za umma Tanzania Bara. Aidha, Tume ya Walimu ina fungu lake (Fungu 2) linalojitegemea na watumishi wake kupitia wasimamizi wao huripoti moja kwa moja kwa Katibu wa Tume ya Utumishi wa Walimu Makao Makuu ya Tume. Hivyo Mamlaka za Serikali za Mitaa hazina bajeti za kuwawezesha uendeshaji wa siku kwa siku wa kazi za TSC zilizoainishwa na sheria kwa kuwa Mamlaka za Serikali za Mitaa ziko chini ya mafungu mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Bunge limeiidhinishia Tume ya Utumishi wa Walimu jumla ya shilingi bilioni 12.515; kati ya hizo shilingi bilioni 4.622 ni matumizi mengineyo ili tume ipate vitendea kazi kama magari, samani za ofisi na pia kugharamia vikao vya mashauri ya nidhamu na rufaa. Hata hivyo, kwa kutambua umuhimu wa Tume, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimewapatia Makatibu Wasaidizi wa Tume katika Wilaya zote nchini Ofisi na baadhi ya vitendea kazi. Serikali itaendelea kuiimarisha Tume ya Utumishi wa Walimu ikiwemo kutatua changamoto za kiutendaji ndani ya wigo wake wa kisheria ili itekeleze majukumu yake vizuri zaidi.
MHE. SEIF K. GULAMALI aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani juu ya suala la kilimo cha umwagiliaji katika Kijiji cha Chomachankola hasa ikizingatiwa kuwa wataalam wa kilimo walikuja kufanya utafiti na kueleza mpango wa kuchimba bwawa kwa ajili hiyo pale Chomachankola?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA K.n.y. WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali hili naomba kwanza nimpe pole Mheshimiwa Jumaa Aweso kwa kufiwa na kaka yake, na pili nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji kwa kunipa heshima ya kuratibu swali hili alipokuwa safarini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji napenda kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali, Mbunge wa Manoga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Chomachankola kina skimu moja ya umwagiliaji inayotumia maji ya Mto Kagon’ho unaotiririsha maji yake msimu wa masika peke yake. Kwenye skimu hii, eneo lililoendelezwa kwa ajili ya kilimo cha mpunga ni hekta 300.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mabadiliko ya tabia nchi ambayo husababisha upungufu mkubwa wa maji wakati wa kiangazi mpango wa Serikali ni kusanifu na kujenga mabwawa madogo na makubwa kwenye maeneo kama kama ilivyo Chomachankola yatakayotumika kuvuna maji ya mvua, kuwezesha kilimo cha umwagiliaji katika vipindi vyote vya mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kijiji cha Chomachankola, Serikali imefanya usanifu wa awali wa bwawa lenye uwezo wa kutunza maji mita za ujazo milioni
(a) Mchakato wa bwawa hilo pamoja na yale ya maeneo mengine yaliyoainishwa kuwa yanafaa kuendelezwa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji katika Wilaya ya Igunga umeingizwa kwenye mpango kabambe wa umwagiliaji utakaoanza kutekelezwa mwaka 2018/2019.
MHE. DAIMU I. MPAKATE (K.n.y. MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI) aliuliza:-
Serikali ya Awamu ya Nne iliahidi kuanzisha Mkoa mpya wa Selous.
a) Je, ahadi hiyo itatekelezwa lini?
b) Je, Serikali haioni kuwa mpaka wa Kusini wenye urefu wa zaidi ya kilometa 600 na wenye mikoa miwili tu sio salama kiulinzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Amandus Ngonyani, Mbunge wa Namtumbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 15 Julai, 2013 Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa ziarani Wilayani Tunduru alikutana na wazee wa Tunduru walioomba mkoa mpya wa Selous. Katika majibu yake alielekeza taratibu zifuatwe kisheria, kwa maana hiyo, hakuahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelekezo hayo, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma imeratibu vikao kadhaa vya kisheria kikiwemo Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Ruvuma cha tarehe 28 Novemba, 2017 kilichosisitiza ombi la kuundwa kwa mkoa mpya wa Selous wenye Wilaya nne za Tunduru, Tunduru Kusini, Namtumbo na Sasawala, Tarafa 10, Kata 53 na Vijiji 212 kwenye eneo lenye kilometa za mraba 38,988 na idadi ya watu 499,913 kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetafakari kwa kina maombi hayo na kuyaona kuwa ni ya msingi. Hata hivyo, kutokana na changamoto ya kuimarisha kwanza miundombinu kama majengo ya Ofisi na nyumba za Watumishi na mahitaji mengine kama vifaa ya Ofisi, Watumishi wa kutosha na vyombo vya usafiri kwenye maeneo mapya ya utawala yaliyoanzishwa tangu mwaka 2010 na 2012, Serikali imesitisha uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala hadi maeneo mapya yaliyopo yaimarishwe kikamilifu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ulinzi na usalama katika mpaka wa Kusini, ipo mikakati ya pamoja baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Msumbiji kuhakikisha kuwa mpaka huo upo salama. Nawaomba wananchi waendelee na shughuli zao bila wasiwasi wowote.
MHE. ALHAJ A. BULEMBO (K.n.y MHE. HUSSEIN N. AMAR) aliuliza:-
Taasisi za umma na taasisi binafsi zimeitikia wito wa Mheshimiwa Rais wa kutengeneza madawati kwa ajili ya shule zetu nchini:-
Je, Serikali na mamlaka husika zimejipanga vipi katika kuhakikisha utunzaji bora wa madawati hayo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang’wale, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inazipongeza na kuzishukuru taasisi zote za umma na za binafsi zilizoitikia wito wa Serikali wa kutengeneza madawati ya kutosha kwa ajili ya shule zetu nchini. Katika kuhakikisha kuwa madawati yaliyotengenezwa kwa ajili ya shule za msingi na sekondari yanatunzwa vizuri na yanadumu kwa muda mrefu, Serikali kupitia Mwongozo wa Matumizi ya Fedha za Ruzuku ya Uendeshaji (Capitation Grants) wa tarehe 28 Desemba, 2015 imeelekeza kuwa asilimia 30 ya fedha hizo itumike kwa ajili ya ukarabati wa samani ikiwemo madawati kwa upande wa shule za msingi na asilimia 10 kwa upande wa shule za sekondari.
Mheshimiwa Spika, aidha, Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa na shule zote wameelekezwa kutotumia madawati hayo kwa shughuli nyingine, kwa mfano, mikutano ya kijiji, vyama vya siasa na matumizi mengine yasiyokusudiwa ili kupunguza kasi ya uharibifu. Ukaguzi wa mara kwa mara umeagizwa kufanyika kwa kushtukiza ili kuhakikisha madawati yaliyopo yanatunzwa vyema.
MHE. SUSAN L. KIWANGA aliuliza:-
Jimbo la Mlimba lina vijana wengi wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari na vyuo lakini wanashindwa kujiajiri kwa kukosa elimu ya ufundi kutokana na jimbo kuwa na kituo kimoja cha ufundi stadi kilichopo Shule ya Msingi Mchombe. Hata hivyo, kituo hicho chenye mahitaji ya walimu sita kina walimu wawili pekee na hakina vifaa. Aidha, kituo kilichopo Shule ya Msingi Mpanga hakina walimu wala vifaa:-
(a) Je, ni lini Serikali itaboresha vituo hivyo vya Mchombe na Mpanga kwa kuwapelekea walimu na vifaa?
(b) Vijana wachache wanaomaliza Kituo cha Mchombe na kufanya mitihani ya NECTA hawapewi vyeti. Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu mzuri katika vituo hivyo ili wawe wanapewa vyeti ili waweze kujiendeleza katika vyuo vya Serikali na kupata madaraja?
(c) Kwa kuwa mitaala ya vyuo vingi imepitwa na wakati, je, Serikali haioni haja ya kuboresha mitaala ya vituo hivyo ili iendane na wakati uliopo kama vyuo vya VETA?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mbunge wa Mlimba lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero imetenga shilingi milioni 10 kwa ajili ya kununulia vifaa na ukarabati wa Kituo cha Ufundi Stadi Mchombe na shilingi milioni 15 kwa ajili ya kufufua Kituo cha Ufundi Stadi Mpanga. Aidha, Serikali inaendelea kubaini walimu waliosomea fani mbalimbali za ufundi ili wahamishiwe kwenye vituo hivi vya ufundi stadi vikiwemo vituo vya Mchombe na Mpanga.
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wanafunzi wanaohitimu mitihani ya NECTA katika vituo vya ufundi vilivyoko kwenye shule za msingi hawajapatiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo hayo tangu mwaka 2015. Aidha, mitaala inayotumika kutoa mafunzo katika vituo vyote 208 ambavyo kwa mwaka 2018 vina wanafunzi 3,000 na walimu 557 ni ya muda mrefu.
Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, Serikali inaupokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge wa kuhakikisha kuwa wanafunzi wanaohitimu mafunzo hayo wanapatiwa vyeti ili wavitumie katika michakato ya kujiendeleza au kazi kwani vijana hao ni sehemu ya nguvukazi katika ujenzi wa uchumi wa viwanda. Kwa kutumia uzoefu uliopatikana hadi sasa, Serikali itaifanyia mapitio mitalaa ya mafunzo hayo ili iendane na mahitaji sasa.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Serikali kupitia Kanuni mbalimbali za Utumishi inatambua mtumishi wa mke au mume na watoto au wategemezi wanne. Hata hivyo, utumishi wa umma hautambui baba wala mama hasa linapotokea tatizo la msiba, mara zote huduma ya misiba ya wazazi imekuwa ni jukumu la mtumishi mwenyewe:-
Je, ni lini Serikali itawajumuisha wazazi wa mtumishi kama wanufaika wa huduma mbalimbali anazopata mtumishi wa umma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH S. KAKUNDA): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma, Toleo la Mwaka 2009, huduma ya mazishi hutolewa kwa mtumishi mwenyewe na wategemezi wanne. Serikali haigharamii mazishi ya baba au mama wa mtumishi kutokana na ukweli kwamba wapo wazazi wenye watoto zaidi ya mmoja katika utumishi wa umma na katika maeneo tofauti nchini. Endapo kwa mfano wazazi wa mtoto zaidi ya mmoja ambao katika utumishi wa umma watafariki Serikali ingelazimika kulipa gharama pengine mara tatu au zaidi kwa kuwa hakuna mfumo madhubuti wa kutambua watu ili kubaini wazazi wenye watoto zaidi ya mmoja katika utumishi wa umma. Kwa kuwa sasa Serikali haina mfumo jumuishi wa utambuzi na udhibiti wa taarifa hizi ingelipa gharama kubwa za huduma za mazishi za mara nne au mara tano au mara tatu kwa mzazi mmoja aliyefariki.
Mheshimiwa Spika, ili kuziba pengo lililopo la kuhudumia mazishi ya wazazi, Serikali imeruhusu watumishi wenyewe kuchangiana kupitia vyama vya hiari ambapo michango yao hufunguliwa akaunti maalum ili inapotokea misiba ya wazazi waweze kupeana rambirambi katika Mifuko ya Kufa na Kuzikana. Kupitia mifuko hii, watumishi wanapofiwa na ndugu zao wa karibu wakiwepo wazazi huwa wanapewa rambirambi. Aidha, huwa kuna michango ya rambirambi ya papo kwa papo inayosaidia gharama za misiba ya watumishi na ndugu wa karibu wakiwemo wazazi, na endapo wazazi wapo mbali na vituo vya kazi watumishi hupewa ruhusa maalum ya siku 14 kushiriki katika misiba.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-
Wilaya ya Lushoto ina hospitali moja ya Wilaya ambayo inabeba mzigo mkubwa sana wa watu. Aidha, wodi ya wajawazito ni chumba kidogo sana na hakuna kabisa wodi ya mama na mtoto. Je, ni lini Serikali itajenga vyumba hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shaabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Hospitali ya Wilaya ya Lushoto bado ina changamoto ya msongamano katika wodi za akina mama wajawazito kwa sababu haina eneo la kutosha kukidhi wingi wa akina mama wajawazito wanaohudumiwa. Wodi ya akina mama wajawazito iliyopo imetokana na uamuzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kubadilisha matumizi ya baadhi ya majengo ili yatumike kama wodi ambapo jumla ya shilingi milioni 30 zilitumika katika mwaka wa fedha 2016/2017 kutengeneza wodi tatu ndogo ndogo yaani wodi ya akina mama wajawazito kabla ya kujifungua, wodi ya akina mama wajawazito baada ya kujifungua yenye uwezo wa kuhudumia akina mama sita kwa wakati mmoja, chumba cha upasuaji chenye vitanda vitatu vya upasuaji na wodi ya akina mama na watoto wachanga baada ya kujifungua kwa kawaida au upasuaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kukabiliana na changamoto hiyo, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imepeleka shilingi milioni 400 katika Kituo cha Afya cha Mlalo; shilingi milioni 500 katika Kituo cha Afya cha Mnazi na shilingi milioni mia tano katika Kituo cha Afya cha Kangagae.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa matumizi ya fedha hizo ni kujenga vyumba vya upasuaji, wodi za mama na mtoto kabla na baada ya kujifungua na maabara kwa lengo la kuboresha huduma kwa mama wajawazito ikiwemo huduma za dharura za upasuaji kwenye maeneo hayo, hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa msongamano kwenye Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa wodi ya kisasa ya wajawazito (maternity complex) ni miongoni mwa vipaumbele vya juu vya Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ndiyo maana katika mwaka wa fedha 2018/2019 imetenga shilingi milioni 25 kuanzisha ujenzi unaotarajiwa kukamilika mwaka 2019/2020.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:- Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya Mwese?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 7 Mei, 2018, Serikali ilipeleka jumla ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga chumba cha mionzi (x-ray), nyumba ya mtumishi, maabara, chumba cha upasuaji, wodi ya mama na mtoto na chumba cha kuhifadhia maiti kwenye Kituo cha Afya cha Mwese katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda. Ujenzi wa kituo hicho unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, 2018.
MHE. ALMAS A. MAIGE aliuliza:-
Zahanati ya Migungumalo, Kata ya Usagari Uyui ilijengwa kwa maandalizi ya kuwa Kituo cha Afya na kufunguliwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa tarehe 25/11/1997 na kuahidi kuwa zahanati hiyo itakuwa Kituo cha Afya cha Kanda ya Magharibi.
(a) Je, Serikali ina mipango gani ya kuikuza zahanati hiyo ili iwe Kituo cha Afya kutokana na mahitaji na huduma zinazotolewa kuwa juu ya uwezo wa zahanati?
(b) Kwa kuenzi kazi na juhudi za Rais Mstaafu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, kufika mpaka Usagari kufungua zahanati; je, Waziri yuko tayari kumwomba Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano kuja kuzindua Kituo cha Afya baada ya kuipandisha hadhi Zahanati hiyo ya Migungumano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Zahanati ya Migungumalo inahudumia wananchi na inatoa huduma za kiwango cha juu. Zahanati hii imeendelea kutengewa fedha kwa ajili ya kutoa huduma za afya kwa wananchi kupitia Mfuko wa Pamoja wa Afya, fedha za matumizi mengineyo, fedha za Benki ya Dunia (RBF), Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) na fedha za dawa kupitia Bohari ya Dawa (MSD). Lengo la Serikali ni kuendelea kuiwezesha zahanati hiyo iendelee kutoa huduma nzuri zaidi kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, miundombinu iliyopo kwa sasa katika Zahanati ya Migungumalo haikidhi vigezo vya kutoa huduma za afya kwa ngazi ya kituo cha afya. Kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kujenga vituo vipya na kuboresha vituo vya afya vilivyopo nchi nzima ili kuimarisha utoaji wa huduma kwa wagonjwa zikiwemo huduma za dharura na upasuaji.
Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali inaendelea na ujenzi wa vituo cha afya 210 kikiwemo Kituo cha Afya cha Upuge ambacho kimepokea shilingi milioni 500 ili kukiwezesha kutoa huduma za dharura na upasuaji. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Tabora/Uyui imetengewa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambayo ikikamilika itahudumia wananchi wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na Serikali ya Wilaya, Halmashauri na viongozi wa Kata ya Usagari ili waanze juhudi za kujenga Kituo cha Afya cha Kata ya Usagari na ikiwezekana waanze juhudi za kujenga zahanati katika kila kijiji kama sera ya afya inavyoelekeza. Serikali iko tayari kuunga mkono nguvu za wananchi katika kumalizia ujenzi huo utakaofanyika chini ya uratibu wa halmashauri, ofisi ya Mbunge na ofisi ya Mkuu wa Wilaya. Kuja kwa Mheshimiwa Rais au kiongozi mwingine wa kitaifa itategemea sana na aina ya miradi itakayokamilika. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. OMAR A. KIGODA) aliuliza:-
Kumekuwa na utekelezaji hafifu wa kusaidia akinamama na vijana kutoka kwenye ile asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri:-
Je, Serikali ina tathmini yoyote ya jinsi gani agizo hilo limetekelezwa kwa kila halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omar Abdallah Kigoda, Mbunge wa Handeni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hufanya ufuatiliaji na tathmini kila robo mwaka, nusu mwaka na mwaka kuhusu utekelezaji wa agizo la kila Halmashauri kutenga asilimia 10 kwa ajili ya vikundi vya vijana na wanawake. Taarifa za ufuatiliaji na tathmini ndizo zimesaidia Serikali kubaini changamoto za usimamizi na uendeshaji unaotokana na upungufu wa kisheria, ikiwa ni pamoja na baadhi ya wanufaika wa mikopo kuwa wagumu kurejesha mikopo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Marekebisho ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2018 yatakayompa Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa nguvu ya kutunga kanuni bora zaidi zitakazolazimisha halmashauri kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo ya akinamama na vijana, Serikali inaamini taratibu za utoaji wa mikopo hiyo, usimamizi na urejeshaji wake zitakuwa nzuri zaidi ukilinganisha na hali ilivyo sasa.
MHE. JOHN P. KADUTU aliuliza:-
Kabla ya kuanzishwa Shule za Kata, kulikuwa na mpango wa kujenga shule katika tarafa. Kwenye Jimbo la Ulyankulu kulijengwa shule tatu ambazo ni Kashishi, Ulyankulu na Mkindo; Shule ya Kashishi hivi sasa ina kidato cha tano na sita:-
Je, ni lini Shule za Mkindo na Ulyankulu zitapewa hadhi ya kuwa na kidato cha tano na sita ili kuwapunguzia wanafunzi gharama za kufuata mbali masomo ya kidato cha tano na sita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Peter Kadutu, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, naomba kwa ruhusa yako niondoe sentensi moja tu inayoanza na neno Tarafa mpaka pale mwisho na sita.
Mheshimiwa Spika, malengo ya Serikali kwa sasa ni kuhakikisha kuwa, kila Tarafa angalau ina shule moja yenye kidato cha tano na sita. Mkakati uliopo kwenye maeneo ambayo tayari kuna shule zinazotoa elimu ya kidato cha tano na sita ni kuziimarisha kwa kuziwekea miundombinu, kuzipatia vifaa vya kufundishia na kujifunzia na kuzipatia Walimu wa kutosha.
Mheshimiwa Spika, ili shule iweze kupandishwa hadhi na hatimaye kusajiliwa kama Shule ya Kidato cha Tano na Sita ni lazima itimize vigezo vifuatavyo:-
(a) Iwe na miundombinu inayojitosheleza kama mabweni, madarasa, bwalo, jiko na maktaba;
(b) Iwe na huduma muhimu na za uhakika za maji na umeme; na
(c) Iwe na Walimu wa kutosha.
Mheshimiwa Spika, kwa muktadha huo, Shule za Sekondari Ulyankulu na Mkindo bado zina changamoto ya miundombinu isiyojitosheleza kama mabweni, madarasa, bwalo, jiko na maktaba. Hivyo, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua ifanye jitihada za makusudi kuwezesha shule hizo mbili kufikia vigezo vinavyohitajika ili ziweze kusajiliwa. Aidha, kwa kuwa bajeti ya Wizara ya Elimu pamoja na ile Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa mwaka 2018/2019 zimeshapitishwa na Bunge, itakuwa vigumu shule hizo kusajiliwa na kuanza kuchukua wanafunzi wa mwaka huo.
MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:-
Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Nyamagana linalojengwa katika Kata ya Mkolani limechukua zaidi ya
miaka minne sasa bila kukamilika:-
(a) Je, Serikali haioni kuwa na miradi isiyokamilika kwa wakati kunarudisha nyuma maendeleo;
(b) Je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha za kukamilsha jengo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa Nyamagana, lenye vipengele (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba ujenzi wa jengo la Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana ulioanza mwaka wa fedha 2008/2009 umechukua muda mrefu. Sababu kubwa ya kuchelewa kukamilika kwa ujenzi huo ni changamoto ya upatikanaji wa fedha za ruzuku ya maendeleo. Hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 1.34 kati ya shilingi bilioni 1.84 zilizokuwa zinahitajika zimetolewa na kutumika katika kujenga boma lenye vyumba 23 vya ofisi, kumbi mbili, mgahawa, chumba cha kuhifadhia nyaraka, vyoo, kuezeka jengo lote, kupiga plasta, kuweka milango, vigae, kupaka rangi, kuweka dari, kufunga milango na madirisha na mfumo wa maji safi na maji taka.
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa kumaliza jengo hilo, jumla ya shilingi milioni 420 zimetengwa katika mwaka wa fedha 2018/2019 ili kumalizia mfumo wa usalama wa jengo ikiwemo zimamoto, mfumo wa umeme, tanki la maji na uzio. Kwa maana hiyo, ujenzi wa jengo hilo unatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2018/2019.
MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza:-
Kituo cha Afya Mlandizi kimetimiza vigezo vyote vya kuwa Haspitali ya Wilaya:-
Je, ni lini sasa Serikali itapandisha hadhi Kituo hicho kuwa Hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Malandizi bado hakijakidhi vigezo vya kukifanya kiwe Hospitali ya Wilaya. Hata hivyo, Serikali haina mpango wa kukipandisha hadhi Kituo hicho kuwa Hospitali ya Wilaya. Serikali imeamua Kituo hicho kiendelee kutoa huduma kama Kituo cha Afya. Hata hivyo, Serikali iliiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha itenge eneo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali Wilaya.
Mheshimiwa Spika, Serikali tayari imeshatenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 1.5 katika mwaka wa 2018/2019 kwa ajili ya ujenzi huo. Pia Halmashauri imeshatenga eneo la ekari 32 lililopo katika Kitongoji cha Disunyala, zamani lilikuwa shamba la United Farming Cooperation kwa ajili ya ujenzi huo.
MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-
Serikali imeanzisha utaratibu wa kutoa elimu bure na kuanza kutekeleza utaratibu huo kwa kupeleka fedha shuleni kidogo kidogo kulingana na idadi ya wanafunzi husika tangu Oktoba 25, 2015:-
(a) Je, Serikali inafahamu kwamba shule nyingi za msingi na za sekondari nchini zikiwemo za Mtwara Mjini zilikuwa na madeni mengi ya wazabuni na steshenari?
(b) Je, Serikali inaweza kueleza kuwa madeni hayo yatalipwa kwa utaratibu upi ikiwa fedha zinazotolewa ni kidogo kwa uwiano wa mwezi kwa mwaka husika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uwepo wa madeni katika shule za msingi na sekondari ambayo yanaanzia mwaka wa fedha 2008/2009 hadi 2016/2017, ikiwa ni madeni ya wazabuni kwa ajili ya chakula cha wanafunzi shuleni na shajara. Katika ya hayo, Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani inadaiwa shilingi milioni 92.4. Madeni hayo ni yale yalikuwepo kabla ya kuanza kwa utekelezaji wa Mpango wa Elimu bila Malipo Desemba, 2015. Kwa sasa, Serikali imejizatiti kutozalisha madeni, ambapo fedha za chakula na mahitaji mengi zinapelekwa kwenye kila shule moja kwa moja kila mwezi. (Makofi)
MHE. JUMA S. NKAMIA aliuliza:-
Shule za Sekondari za Farkwa na Msakwalo zilizoko Wilayani Chemba zimepandishwa hadhi kuwa za A – level na idadi ya wanafunzi imeongezeka katika shule hizo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipatia maji ya uhakika shule hizo ili kuwaondolea wanafunzi adha ya kutafuta maji badala ya masomo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Selemani Nkamia, Mbunge wa Chemba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Sekondari Msakwalo ilikuwa ikitumia maji ya bomba kutoka katika kisima cha kijiji na Shule ya Sekondari Farkwa ilikuwa inatumia miundombinu ya kuvuna maji ya mvua na pia ilikuwa ikitumia maji ya bomba kutoka katika kisima cha kijiji. Visima hivi pamoja na uchakavu wa miundombinu havikuwa na uwezo wa kuzalisha maji ya kutosha kwa matumizi ya vijiji pamoja na shule. Hivyo, shule hizo kushindwa kupata maji ya kutosheleza kwa mwaka mzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua tatizo la maji katika Shule za Sekondari Msalikwa na Farkwa, Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018, ilitoa jumla ya shilingi milioni 104 kwa Shule ya Sekondari Msalikwa na shilingi milioni 87 kwa Shule ya Sekondari Farkwa kwa ajili ya kuchimba visima na kufanya ukarabati wa miundombinu ya mfumo wa bomba kwenye shule hizo. Kazi ya uchimbaji wa visima na ukarabati wa miundombinu ya mabomba katika shule hizo imekamilika na wanafunzi kwa sasa wanapata maji ya kutosha.
MHE. MICHAEL J. MKUNDI - (K.n.y MHE. WILFRED M. LWAKATARE) aliuliza:-
Kukua kwa elimu ya uraia na ufahamu wa mambo ya kisiasa kumefanya wananchi wengi kuupokea mfumo wa vyama vingi na kuchagua wawakilishi wengi wa Vyama vya Upinzani kuongoza Kamati za Maendeleo za Kata, Halmashauri za Miji, Miji Midogo, Wilaya, Manispaa, Majiji na Majimbo ya Ubunge na Udiwani:-
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kutengeneza kanuni, utaratibu na mfumo wa kutoa elimu na maelekezo kwa watendaji na viongozi wa Kiserikali kuyakubali na kupata ufahamu wa mabadiliko ya kisiasa yanayokua kwa kasi ili kuepusha migogoro na migongano ya usimamizi wa kazi baina ya watendaji wa Serikali na wawakilishi wa wananchi?
(b) Je, kwa nini Serikali isiweke utaratibu wa kuwa na uchaguzi huru na haki kama vile Tume Huru ya Uchaguzi na chombo huru cha kusimamia chaguzi za vitongoji, vijiji na mitaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kwanza uniruhusu nimsahihishe kidogo Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali kwa niaba, huyu Mheshimiwa haitwi Alfred Lwakatare anaitwa Wilfred Lwakatare. Naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Wilfred Lwakatare, Mbunge wa Bukoba Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, watendaji na viongozi wa Serikali wanafanya kazi kwa mujibu wa Katiba, Sheria, Kanuni, Taratibu na miongozo iliyopo. Ni wajibu wa viongozi na watumishi wote katika ngazi zote za Serikali kuzifahamu nyenzo hizo za kazi ili kuepusha migogoro na migongano baina yao. Serikali imekuwa ikiwaongezea uwezo wa kiutendaji na uongozi watendaji na viongozi wao kupitia mafunzo ya mara kwa mara na vikao vya kazi ili wawahudumie wananchi vizuri na kwa tija zaidi.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa, Mamlaka za Wilaya na Mamlaka za Miji, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa husimamia uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa ambao hufanyika ukiwa huru na haki kila baada ya miaka mitano kwa kushirikisha wadau wote wakiwemo viongozi wa vyama vya siasa ambao hutoa maoni yao kunzia kwenye maandalizi ya uchaguzi.
MHE. ISSA A. MANGUNGU aliuliza:-
Serikali ilikuwa na utaratibu wa kutoa Posho ya Kufundishia (Teaching Allowance) lakini kwa sasa imefutwa:-
(a) Je, ni kwa nini Serikali iliifuta posho hiyo?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuirejesha posho hiyo?
(c) Katika Jimbo la Mbagala, shule nyingi hazina nyumba za walimu; mfano, Shule za Msingi Mbagala, Maji Matitu na Rangi Tatu. Je, ni lini Serikali itatatua kero hii kwa mkakati maalum kama ilivyoweka mkakati wa upatikanaji wa madawati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ali Mangungu, Mbunge wa Jimbo la Mbagala, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haikufuta Posho ya Kufundishia bali iliijumuisha katika mshahara wa mwalimu kwa lengo la kuongeza kiwango cha fedha (pensheni na kiinua mgongo) baada ya kustaafu. Awali posho hiyo ilikuwa inatolewa kwa watumishi nje ya mshahara, hivyo, haikuwa sehemu ya kikokotoo cha mafao ya watumishi baada ya kustaafu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua upungufu wa nyumba za walimu uliopo katika maeneo yote mijini na vijijini. Hata hivyo, kutokana na urahisi wa walimu na watumishi wengine wa Serikali kupata nyumba za kupanga maeneo ya mjini kama ilivyo katika Manispaa za Jiji la Dar es Salaam, kipaumbele cha juu cha ujenzi wa nyumba za walimu kimewekwa zaidi katika maeneo ya vijijini kule ambako kuna mazingira magumu ya kupata nyumba za kupanga ili kuboresha mazingira ya kufanyia kazi kwenye maeneo hayo.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-
Tunapoelekea kujenga uchumi wa viwanda ni wazi kuwa fursa za kibiashara zinazojitokeza nyingi zitafanywa na wajasiriamali wadogo; hata hivyo muundo wa kazi kwa kada ya Maafisa Biashara katika Halmashauri zetu umefichwa ndani ya Idara ya Fedha, pamoja na kazi na uzito wa majukumu ya biashara siyo idara wala kitengo:-
Je, ni lini Wizara kwa kushirikiana na Utumishi itafanya kada hii kutambulika kwa uzito wake ili wanufaike na uwepo wa Maafisa Biashara kuliko ilivyo hivi sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika muundo wa sasa wa Mamlaka za Serikali za Mitaa ulioidhinishwa mwaka 2011 wenye Idara 13 na Vitengo Sita, kada ya Maafisa Biashara ipo ndani ya Idara ya Fedha na Biashara. Napenda kulialifu Bunge lako Tukufu kuwa hivi sasa Serikali inaufanyia mapitio ya kina muundo huo kwa kuzingatia uzito wa kazi kwa kila kada ili kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za uendeshaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Cosato David Chumi kwa kuwa maudhui ya swali lake yamechangia mawazo mazuri katika mapitio ya muundo wa Serikali za Mitaa yanayoendelea.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza:-
Hali ya barabara zinazosimamiwa na halmashauri ni mbaya sana kutokana na fedha zinazotolewa na Mfuko wa Barabara kukaa kwa muda mrefu na hali ya kuongezeka kwa magari binafsi na yale ya biashara ambapo kila tarafa ina zaidi ya magari 20 na hivyo, kufanya barabara hizo kuharibika na kuwa vigumu kupitika nyakati za masika:-
(a) Je, Serikali haioni haja ya kuleta mapendekezo mapya ya mgao wa fedha za barabara?
(b) Barabara nyingi za Halmashauri ya Mji wa Mbulu zimejifunga katika Tarafa za Nambis na Daudi. Je, kwa nini wataalam kutoka Wizarani wasifike kuzikagua na kutoa ushauri stahili?
(c) Je, kwa nini BQ za tenda za barabara ngazi ya mkoa zisiwekwe kwenye kitabu cha RRB, ili Waheshimiwa Wabunge na wananchi wafahamu shughuli zitakazofanywa na makandarasi waliopewa kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paul Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, lenye Sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kufanya tathmini ya mtandao wa barabara nchi nzima ili hatimaye utumike kuangalia kwa kina utaratibu mzuri zaidi wa mgawo wa fedha za barabara kati ya TANROADS inayoshughulikia barabara kuu na barabara za mikoa na TARURA inayoshughulikia barabara za Mamlaka za Serikali za Mitaa.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2017/2018 Barabara za Mji wa Mbulu zilitengewa shilingi milioni 814.56. Kati ya hizo shilingi milioni 262.12 zilitengwa kwa ajili ya barabara kwa ajili ya matengenezo ya muda maalum (Periodic Maintenance) Barabara za Ayamaame – Kainam – Hhasama – Mbulu – Endagikot – Tlawi, Tango FDC, Waama – Masieda, Ayayumba – Hhayloto zenye urefu wa kilometa 35.7 katika Tarafa za Daudi na Nambisi na kuweka changarawe katika Barabara za Ayamaami – Kainam – Hhasama, Mbulu – Kuta na Ayayumba - Hhayloto zenye urefu wa kilometa 8.13
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuchonga barabara ya Uhama – Masieda – Hayayumba – Hailoto zenye urefu wa kilometa 31.5 na ujenzi wa kalavati za njia mbili zenye kipenyo cha milimita 900 katika Tarafa ya Daudi. Barabara zilizokuwa zimejifunga kwa kuharibika na mvua sasa zinapitika ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 95 na kazi inaendelea. Katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 Barabara za tarafa za Nambis na Daudi zimetengewa shilingi milioni 438.8 kwa ajili ya matengenezo.
c) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni haki ya wajumbe wa Bodi ya Barabara ya Mkoa na wananchi kupata taarifa za jumla za barabara zilizopangwa kujengwa katika mkoa, ikiwemo gharama za kazi ambazo wajumbe wanaweza kuzipata katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Barabara ya Mkoa.
MHE. ENG. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara inayounganisha Kata ya Haneti na Kata ya Segala kupitia Kata ya Zajilwa ni muhimu sana kwa kufungua mawasiliano katika kata hizo tatu:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa barabara hiyo, inatengenezwa kwa kiwango cha kupitika muda wote kwa mwaka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha, 2017/2018 Serikali ilitenga na ilitoa fedha zote shilingi milioni 132.1 ambazo zimetumika kufanya matengenezo, si tu kwenye barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge bali barabara ndefu zaidi ya kutoka Segala – Zajilwa – Haneti – hadi Umoja yenye urefu wa kilometa 80. Barabara hiyo, imekamilika na sasa inapitika muda wote wa mwaka.
MHE. BONIPHANCE M. GETERE aliuliza:-
Mnamo tarehe 12 Januari, 2018 Jeshi la Polisi lilifanya msako mkali katika Kijiji cha Mekomario – Bunda na katika msako huo wananchi wa eneo hilo waliharibiwa mali zao kama ilivyothibitishwa na Mkuu wa Wilaya ya Bunda na kutangazwa kwenye vyombo vya habari yaani Star TV tarehe 15 Februari, 2018:-
Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya kulipa fidia wananchi kutokana na uharibifu huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ambaye anaongoza Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa na Wilaya, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 12 Januari, 2018 zilienezwa tetesi katika Kijiji cha Mekomariro, Wilayani Bunda kwamba wezi kutoka katika Kijiji cha Remong’oroni, Wilayani Serengeti walikuwa wameiba mifugo ya wakazi wa Mekomariro. Badala ya kutoa taarifa Polisi ili wasaidiwe kitaalam kupitia uchunguzi wa Polisi kubaini walioibiwa na idadi ya mifugo iliyoibiwa, walijikusanya kwa utaratibu usiokubalika na kwenda katika Kijiji cha Remong’oroni, wakafanya vurugu zilizosababisha watu wawili wakazi wa Kijiji cha Remong’oroni kuuwawa kikatili na wakamteka mtoto mmoja wa kiume.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa za ghasia hizo ziliporipotiwa Polisi, msako ulifanyika kuwabaini wahusika ambapo watuhumiwa nane wamefunguliwa mashtaka Mahakamani kwa kesi ya mauaji Na. RM 02/2018 ambayo bado inaendelea. Msako uliofanyika pamoja na ule wa watuhumiwa wengine waliojificha unaoendelea haujasababisha uharibifu wa mali za wananchi wa Mekomariro wala wa Remong’oroni. Kwa kuwa kesi inaendelea, nashauri tusubiri uamuzi wa Mahakama ili tupate ufumbuzi wa kisheria wa suala hilo.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y. MHE. DKT. DAVID M. DAVID) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapeleka waganga, watumishi wa afya pamoja na vitendea kazi katika zahanati za Same Magharibi zilizojengwa kwa ushirikiano wa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt.David Mathayo, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua tatizo la upungufu wa watumishi wa sekta ya afya katika Jimbo la Same Magharibi, ambapo mahitaji ni watumishi 867 lakini waliopo ni 287, upungufu ni watumishi 585.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imepeleka watumishi wapya 10 wa sekta ya afya katika jimbo hilo. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Halmashauri ya Wilaya ya Same imeomba kibali cha kuajiri watumishi wapya 104 wa sekta ya afya ambao watapangwa katika vituo vyenye upungufu mkubwa wa watumishi.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA aliuliza:-
Serikali inaanzia katika ngazi ya kitongoji, mtaa na kijiji:-
Je, ni lini viongozi na Wenyeviti wa Vitongoji, Mtaa na Kijiji watalipwa mishahara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniventura Destery Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa sifa zinazomwezesha Mtanzania kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kijiji, Kitongoji au Mtaa ni pamoja na kuwa na shughuli halali inayomwingizia kipato. Kwa muktadha huo, utaratibu wa viongozi kwa ngazi hiyo kulipwa mishahara kama ilivyoulizwa katika swali la msingi haujawahi kuwekwa kwenye sheria yoyote.
HASNA S. K. MWILIMA aliuliza:-
Jimbo la Kigoma Kusini lenye ukubwa wa kilometa za mraba 10,178 lina jiografia mbaya na idadi ya wakazi wake ni kubwa sana:-
a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuligawa jimbo hilo na kuanzisha halmashauri nyingine ili kuwarahisishia wananchi kupata huduma za kijamii kiurahisi?
b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha Mamlaka ya Mji Mdogo katika Tarafa ya Nguruka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali refu la Mheshimiwa Hasna Sudi Katundu Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imepewa mamlaka ya kuyagawa majimbo ya uchaguzi kwa kuzingatia vigezo vya idadi ya watu, jiografia, hali ya mawasiliano, ukubwa wa jimbo na uwezo wa ukumbi wa Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Jimbo lolote ligawanywe, Tume hutoa tangazo kuhusu nia hiyo. Baada ya tangazo, mapendekezo hujadiliwa katika vikao vya Halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa na hatimaye kuwasilishwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo hutangaza jimbo jipya baada ya kupata kibali cha Rais.
• Mheshimiwa Mwenyekiti, vigezo vinavyozingatiwa katika kuanzisha Mamlaka za Miji Midogo ni pamoja na idadi ya watu wasiopungua elfu hamsini, kata zisizopungua tatu, eneo lisilopungua kilomita za mraba mia moja na hamsini, viwanja vilivyopimwa visipungue asilimia
30 ya eneo lote, uwepo wa mpango kabambe wa uendelezaji wa mji (master plan) na huduma za jamii za kukidhi ukuaji wa mji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, mapendekezo ya kuanzisha Mamlaka ya Mji Mdogo yanapaswa kuanzia kwenye Mkutano Mkuu wa Kijiji, Kamati ya Maendeleo ya Kata, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa kwa kuzingatia vigezo hivyo kwa mujibu wa sheria. Mapendekezo ya vikao hivyo huwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kumshauri ipasavyo Waziri mwenye dhamana.
MHE. CATHERINE N. RUGE aliuliza:-
Bado kuna kata ambazo hazina shule za sekondari hivyo kufanya baadhi ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kwenda na kurudi shuleni, kutokana na hali hiyo baadhi ya wazazi wameamua kuwapangishia vyumba watoto wao mitaani kwenye mazingira ambayo si salama.
Je, kwa nini Serikali isije na mpango mahususi wa ujenzi wa mabweni kama inavyofanya kwenye madawati ili kuwapunguzia wanafunzi hasa wa kike adha ya kutembea umbali mrefu kwenda na kurudi nyumbani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI napenda kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Nyakao Ruge, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inamiliki na kuendesha shule za sekondari 3,634 Tanzania Bara. Kati ya hizo shule 3,519 ni za kutwa na shule 155 ni za bweni. Idadi hiyo ukiilinganisha na kata 4,420 inabainisha kuwepo na kata ambazo hazina shule za sekondari hivyo zipo changamoto za baadhi ya wanafunzi kutembea umbali mrefu kufuata shule kwenye kata za jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pendekezo la Mheshimiwa Mbunge la kujenga mabweni katika shule zote sekondari kuwa zuri, Serikali imeweka kipaumbele kujenga mabweni kwanza kwenye shule za kidato cha tano na sita pamoja na zinazoandaliwa kupandishwa hadhi kuwa za kidato cha tano na sita ambazo husajili wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi. Tangu mwaka 2014 Serikali imetumia shilingi bilioni 29.4 kujenga mabweni 298 kwenye shule za sekondari na mabweni 25 kwenye shule za msingi.
Aidha, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imepanga kutumia jumla ya shilingi bilioni 15.7 kujenga mabweni 206 katika shule za sekondari na mabweni manne katika shule za msingi. Halmashauri zinahimizwa kuendelea kushirikiana na wananchi na wadau wengine kujenga shule za sekondari kwenye kata ambazo hazina shule na kujenga dahania (hostel) kwenye shule za sekondari zenye wanafunzi wanaotembea umbali mrefu.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Hali ya sekta ya kilimo na mifugo katika Jimbo la Same Mashariki ni mbaya licha ya kuwepo wafanyakazi wa Serikali wanaosimamia sekta hizo kwenye Wilaya, Kata na hata Vijiji. Wengi wa wafanyakazi hao wanatumia muda mwingi kufanya kazi zao binafsi badala ya kuwasaidia wakulima na wafugaji kuleta mabadiliko katika sekta hizo.
(a) Je, Serikali inatumia kigezo gani kutathmini utendaji kazi wa waajiriwa hao kupima ufanisi wao?
(b) Je, Serikali ipo tayari kupunguza idadi ya waajiriwa hao waliopo vijijini ili fedha itakayookolewa kutoka katika mishahara yao isaidie kutengeneza miundombinu ya umwagiliaji na malambo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuwasimamia maofisa ugani kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wizara za Kisekta hutoa miongozo inayoainisha viwango vya kitaalam na ikama. Mamlaka za Serikali za Mitaa husimamia masuala ya kiutawala na utendaji kazi wa siku kwa siku ikiwemo kupima ufanisi na tija kwa kutumia Mfumo wa Wazi wa Upimaji wa Watumishi wa Umma (Open Performance and Review Appraisal System – OPRAS) ambapo kila mtumishi hukubaliana na mwajiri kuhusu malengo yatakayotekelezwa kwa mwaka mzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa bado kuna upungufu mkubwa wa maafisa ugani wa kilimo na mifugo nchini, badala ya kupunguza idadi yao, mpango uliopo kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 22(b) ni kuongeza idadi ya Maafisa Ugani kutoka 9,558 waliokuwepo mwaka 2014 hadi 15,082 ifikapo mwaka 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwakumbusha maafisa ugani wote na wasimamizi wao kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu yaliyowataka Maafisa Ugani kutokaa ofisini na badala yake kwenda vijijini kuwasaidia wakulima na wafugaji. Nazikumbusha mamlaka za nidhamu kuchukua hatua kali dhidi ya Maafisa Ugani wazembe wasiowajibika kwa umma.
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA aliuliza:-
Mji Mdogo wa Bagamoyo ulianzishwa tarehe 15/6/ 2005. Mwaka 2013/2014 Mamlaka hiyo iliiomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupewa hadhi ya Halmashauri ya Mji baada ya kujiridhisha kuwa na sifa stahili.
Je, ni lini Serikali itaipa Bagamoyo hadhi ya kuwa Halmashauri ya Mji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria za Serikali za Mitaa Sura 287 (Mamlaka za Wilaya) na Sura 288 (Mamlaka za Miji), pamoja na mwongozo wa Serikali kuhusu uanzishwaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wa Mwaka 2014, mapendekezo ya kupandisha hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo kuwa Halmashauri ya Mji yanapaswa kujadiliwa kwanza kwenye kikao cha Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kabla ya kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa uamuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa maombi hayo yalijadiliwa katika Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo tarehe 28, Septemba, 2018 (mwaka huu), na Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) tarehe 06, Oktoba, 2018 na kwa kuwa hayajajadiliwa kwenye Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) ambao wamepanga kikao hivi karibuni, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inamuomba Mheshimiwa Mbunge awaarifu wadau wa Mji wa Bagamoyo wawe na subira hadi taratibu hizo zitakapokamilika na uamuzi kufikiwa.
MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA aliuliza:-

Seikali ina mkakati gani wa kujenga Kiwanda cha Kusindika Nyanya katika maeneo ya Mto Ngarenanyuki?
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kufanya marekebisho kidogo ya Kiswahili sanifu kwenye majibu yangu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Stephen Lemomo Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kuwa eneo la Mto Ngarenanyuki katika Wilaya za Arumeru na Longido ni miongoni mwa maeneo yanayolimwa nyanya kwa wingi nchini. Ndiyo maana kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo tumeendelea kuweka mazingira wezeshi sambamba na kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya kusindika nyanya. Kwa kuwa ni muhimu kwa kiwanda kuwa na uhakika wa malighafi za kutosha mwaka mzima namwomba Mheshimiwa Mbunge tuendelee kushirikiana kuhamasisha uzalishaji zaidi wa nyanya ikiwezekana zipatikane kwa mwaka mzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kupita SIDO imekuwa ikitoa mafunzo ya aina mbalimbali kuhusu ujasiriamali na usindikaji wa mazao ya kilimo. Naomba wananchi wa eneo wa Mto Ngarenanyuki katika Wilaya hizo mbili na Wilaya nyingine nchini waitumie fursa hiyo kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya kusindika mazao ikiwemo nyanya.
MHE. SONIA J. MAGOGO (K.n.y. MHE. MUSSA B. MBAROUK) aliuliza:-

Wakazi wa Kata ya Kirare, Tongoni, Mzizima, Chongoleani, Mabokweni na Pongwe Wilayani Tanga Mjini ni wazalisaji wakubwa wa zao la muhogo lakini hawana soko la uhakika:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutafuta soko la uhakika wa zao la muhogo ndani na nje ya nchi?

(b) Zipo mashine za kuchakata muhogo lakini bei zake ni kubwa na hivyo wakulima hawana uwezo wa kununua; je, Serikali haioni haja ya kuondoa kodi katika mashine hizo?
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, imeweka vipaumbele vitatu ambavyo ndivyo tunavyoviwekea msisitizo wa uwekezaji kwenye sekta ya viwanda. Vipaumbele hivyo ni viwanda vya kusindika mazao ya kilimo ili kuongeza thamani sambamba na kulinda jasho la mkulima; viwanda vya kutengeneza bidhaa za majumbanii kama vyakula, nguo, mafuta ya kula, samani na kadhalika na bidhaa tegemezi kwenye sekta ya ujenzi kama sementi, mabati na kadhalika ili kuharakisha ubora wa maisha na maendeleo; viwanda vinavyoajiri watu wengi kwa ajili ya kuhakikisha ajira kwa vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la muhogo ambalo ni maarufu kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Lindi, Mtwara na maeneo mengi ya nchi hadi Kigoma kwa sasa limepewa kipaumbele maalum duniani. Kutokana na ukweli kwamba muhogo hausindikwi kutengeneza unga wa ugali au uji au mkate au biskuti peke yake bali unga wa muhogo unatumika kwa sasa kwenye uunganishaji wa chuma, mbao, kutengeneza gundi na matumizi mengine mengi sana. Soko la muhogo Ulaya, Marekani na China ni kubwa sana kwa sasa. China peke yake inahitaji tani milioni mbili na nusu za muhogo kwa mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ukweli huo, kasi ya ujenzi wa viwanda vya kusindika muhogo ni kubwa. Mwaka huu peke yake ukiacha viwanda vitano vinavyonunua muhogo wa mkulima kwa sasa kikiwemo kile kilichopo Handeni, viwanda viwili vipya vitakuwa vimefunguliwa kabla ya Juni, 2019 kimoja Lindi na kingine Pwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu bei kubwa za mitambo kutoka nje, nawashauri wawekezaji wa ndani watembelee SIDO na TEMDO kwanza maana ni taasisi za ndani ambapo miongoni mwa majukumu yake ni kubuni na kutengeneza mitambo na mashine za kusindika mazao zenye gharama nafuu. Endapo italazimika kuagiza nje ya nchi, italazimu kufuata Sheria ya Fedha iliyopo au kusubiri mapendekezo yaliyopelekwa kwenye Kikosi Kazi cha kutathmini mapendekezo ya marekebisho ya kodi yatakayojadiliwa wakati wa kujadili rasimu itakayoletwa na Serikali Bungeni Juni, 2019.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-

Serikali ya Tanzania ni mdau mkubwa wa Mradi wa Bomba la Mafuta ghafi kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga na Serikali pamoja na wawekezaji katika mradi huu walishateua eneo la kujenga kiwanda cha kuunganisha na ku-coat mabomba katika Mji Mdogo wa Isaka.

Je, ni hatua gani imefikiwa katika ujenzi wa kiwanda hicho?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi kutoka Hoima (Uganda) hadi Tanga (Tanzania) linalojulikana kama bomba la Afrika Mashariki (East Africa Crude Oil Pipe – EACOP Project) umeainisha maeneo ya ardhi kwa ajili ya kazi za awali. Maeneo hayo yanazingatia vipaumbele vya mradi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya kiwanda cha upigaji rangi mabomba uliopo kati ya Kijiji cha Sojo, Kata Igusule, Wilaya ya Nzega, Mkoa wa Tabora karibu na eneo la reli inayoenda Isaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa kiwanda hicho muhimu katika mradi wa bomba utaanza mara tu baada ya kukamilika kwa zoezi la kuthaminisha na kutoa ardhi husika na kukabidhiwa mkandarsi wa ujenzi. Kwa sasa, taratibu za utoaji ardhi ziko katika hatua za mwisho na zinatarajia kukamilika mapema mwezi Julai, 2019. Mkandarasi anatazamia kukabidhiwa eneo la mradi na kupeleka vifaa mwezi Septemba 2019. Aidha, mpango wa usimamizi wa mazingira na jamii umekamilika na kuidhinishwa na Baraza la taifa la usimamizi wa mazingira NEMC.