Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Hussein Mohamed Bashe (209 total)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Sina sababu ya kumjibu rafiki yangu Mheshimiwa Bashe kwa sababu alikuwa mwenzetu huku alikuwa anazijua vizuri takwimu.

Mheshimiwa Spika, nilichokisema ni sahihi. Swali langu la kwanza hivi viuadudu tunapokuwa tumelima pamba vinakuja wakati ambapo siyo sahihi na vinapokuja vingine vime- expire. Hizi takwimu anazozisoma Mheshimiwa Bashe ni takwimu za makaratasi. Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari tutakapomaliza Bunge hili twende kwa wananchi wangu wa Kijiji cha Rubanga, Isirwabutondwe, ukajionee madhara waliyoyapata kipindi kilichopita?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika msimu wa pamba 2018/2019 kumeingia mdudu anaitwa ushirika na Waziri anaufahamu kabisa. Tumekuwa na matatizo makubwa sana kati ya mkulima na wanunuzi wa pamba uliosababishwa na ushirika. Yote haya yamesababishwa na Serikali kutokutusikiliza sisi wakulima. Ushirika ni chombo ambacho kimetuvuruga sana wakulima wa pamba pamoja na kwake Mheshimiwa Bashe miaka ya nyuma lakini Serikali ilichukua uamuzi wa kusema sasa ushirika lazima ununue pamba kwa bei inayotaka ushirika. Sasa Mheshimiwa Waziri nilikuwa nauliza kwa sababu Serikali inautambua ushirika na una asset zake ambazo zinaweza kukopeshwa benki, mko tayari sasa kutoa kauli kwamba wakope hela bank ili waingie kwenye ushindani na makampuni mengine ili msimu ujao kusitokee vurugu iliyotokea mwaka huu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba ni ukweli usiofichika kwamba wakulima wa pamba kwa muda mrefu wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kupewa baadhi ya viuadudu vikiwa chini ya kiwango. Sisi kama Wizara ya Kilimo tumeamua kwamba katika msimu wa mwaka huu ambao sasa hivi wakulima wamelima viuadudu vyote vitakavyosambazwa msambazaji atasaini mkataba wa quality assurance ili pale ambapo atapeleka kiuadudu ama dawa itakuwa na tatizo la ubora atakuwa heard responsible na kushtakiwa kwa uhujumu uchumi kwa sababu kile ni kitendo cha kuhujumu uchumi wa mkulima na taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, lakini mbali na hapo, tumewataka wasambazaji wote ambao wataingia makubaliano ya kusambaza dawa hizi wahakikishe wana-provide extension services. Kwa sababu si sahihi kwenda ku-damp dawa katika go-down bila kushiriki katika zoezi la kutoa elimu ya usambazaji na upulizaji wa dawa. Kwa hiyo, usambazaji katika msimu huu utaendana pamoja na makubaliano juu ya suala la ubora na yeyote atakayesambaza dawa ambayo itakuwa chini ya ubora atachukuliwa hatua za kisheria na business as usual katika suala la dawa halitakuwepo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la ushirika, kwanza kuhakikisha ushirika unajengwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Serikali iliyoko madarakani inasimamia utekelezaji wa ilani wa chama kilichopo madarakani. Ni sahihi kwamba kumekuwepo na viongozi wa ushirika ambao siyo waaminifu. Tatizo hili si tu linasababishwa na ushirika lakini vilevile wako baadhi ya wanunuzi wa pamba na Mheshimiwa Musukuma anawajua na sisi wote tunajua kwamba wanafanya mchakato wa kuvuruga mfumo ili waweze ku-benefit.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Serikali tumeamua safari hii kwanza ushirika haununui pamba anayenunua pamba ni mfanyabiashara binafsi. Tunachokifanya ni kwamba tunatumia Ushirika na Vyama vya Msingi ili wakulima waweze kukusanya pamba yao sehemu moja na kupitia ushirika kudhibiti suala la ubora ambalo linaathiri zao la pamba katika soko la dunia. Msimu huu haujasababishiwa matatizo yake na ushirika msimu huu bei ya pamba imekumbwa na tatizo katika soko la dunia.

Mheshimiwa Spika, msimu ujao kutakuwa hakuna malipo ya cash, wakulima wote watatakiwa wawe bank account, Vyama vyote vya Msingi vitakuwa na bank account na wafanyabiashara wote watalipa fedha za wakulima kupitia bank account. Hivi tunavyoongea bank ya CRDB na NMB wanazunguka vijijini kuwafungulia wakulima wa pamba akaunti bila gharama. Akaunti zao zitakuwa bure ili msimu ujao tusikumbane na matatizo yaliyotokea katika msimu huu.

Mheshimiwa Spika, lakini niwaombe Waheshimiwa Wabunge na ninyi mshiriki katika suala la kuhakikisha katika ngazi za AMCOS viongozi wanaopatikana ni waaminifu ili waweze kusimamia vyama vya ushirika na kuweza kufikia lengo la Serikali kujenga ushirika uliokuwa imara.
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana. Nimemsikiliza vizuri sana Mheshimiwa Naibu Waziri. Swali langu ni dogo sana, kwa sababu sasa wakulima wa pamba tayari wameshalima pamba yao lakini tatizo lililopo hivi sasa hakuna viuadudu ambavyo vimeshapelekwa. Bwana Waziri wewe, najua wewe ni champion wa pamba, ni lini dawa za kuua wadudu zitapekwa kwa wakulima wetu wa zao la pamba?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, nataka nimjibu Mheshimiwa Senata Ndassa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hivi sasa tunavyoongea usambazaji wa viuadudu umeanza katika maeneo ambayo wakulima walianza kulima mapema mwezi Oktoba, katika baadhi ya Wilaya za Mkoa wa Geita. Mpaka sasa tumeshasambaza chupa laki tisa na zoezi la usambazaji linaendelea.

Mheshimiwa Spika, lakini kutokana na kalenda tutahakikisha viuadudu vinafika kwa wakati. Kwa mujibu wa kalenda wakulima wanatakiwa kupulizia mara ya pili kuanzia tarehe 15 Februari, tunahakikisha kwamba wakulima wote watapata dawa kwa wakati. Ndani ya Serikali na Bodi ya Pamba mchakato unaendelea na taasisi za fedha zimeshajitokeza kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana.

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge hili kuomba, kilimo cha pamba kwa miaka yote kimeendelea kutegemea mgogo wa Serikali. Pamba ni zao ambalo limelimwa kwa muda mrefu likitegemea kubebwa na Serikali. Niombe na nitumie nafasi hii umewadia wakati wa zao la pamba kusimama lenyewe, dawa ziuzwe katika maduka kama wakulima wengine wanavyopata, mbegu zipatikane na sisi kama Serikali tunajenga huo mfumo ili bidhaa hizi zisiwe tena mpaka zitengemee intervention ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, tumekubaliana hakuna dawa wala mbegu ya bure. Nitumie Bunge hili kulisema hili wazi, vikao vya wadau tumekaa tumekubaliana wakulima wanakopeshwa mbegu na wameshakopeshwa wamelima, safari hii watakopeshwa viuatilifu na mwisho wa msimu kila mkulima atakatwa Sh.150 ili kulipia mbegu walizokopeshwa safari hii jumla ya tani 24,000 na viuadudu na viuatilifu watakavyokuwa wamekopeshwa katika kipindi hiki cha kupulizia dawa. Kwa hiyo, nimtoe hofu kuanzia tarehe 15 wakulima watakuwa katika nafasi nzuri ya kupata dawa husika.
MHE. MARGARETH S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Hussein Bashe kwa kupewa nafasi kubwa kama hivyo hongera sana Mheshimiwa. Pia nampongeza kwa majibu aliyoyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yangu ya nyongeza yako kama ifuatavyo: Kwanza hadi leo hii kuna tani 12 za tumbaku ambazo hazijanunuliwa na wakati huo msimu wa kilimo umeshafika, baadhi ya kampuni hazijatoa makisio hadi leo hii. Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha kwamba tumbaku yote inanunuliwa na makisio yanapatikana?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuna taarifa kwamba kampuni ya TLTC ambayo ilikuwa ikinunua tumbaku Kilograms 16 milioni ilikuwa na viwanda vya tumbaku, ilikuwa na maghala na wakati huo ilikuwa na wafanyakazi 300 ambao sasa kampuni hii ikijitoa ni kwamba hawa wafanyakazi wanapoteza kazi. Je, Serikali inachukua hatua gani ili kuhakikisha kwamba hii kampuni pamoja na kuondoka, Serikali inatoa kauli gani kwamba TLTC ikitoka itakuwaje sasa kwa sababu ndiye ilikuwa mnunuzi mkubwa na kama nilivyosema ilikuwa na maghala, viwanda na wafanyakazi 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatoa kauli gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri kwamba kuna tumbaku mikononi mwa wakulima kiasi cha kilo milioni 12, hili jambo la fact na ni ukweli. Serikali imechukua hatua zifuatazo:

Mheshimiwa Naibu Spika, kampuni ambazo zimekuwa zikinunua tumbaku zimekuwa zikipitia changamoto mbalimbali. Changamoto zingine zinasababishwa na uzembe wa baadhi wa Watendaji katika Serikali, kama Wizara tumechukua hatua, jana tumekutana na kukubaliana na kampuni nne zote za tumbaku ambazo zinanunua tumbaku nchini ambazo zilionesha nia ya kutokununua tumbaku hizo ambazo ziko mkononi mwa wakulima, tarehe 12 Council ya Tobacco takutana na kampuni hizi ili tumbaku hizo kuondoka mikononi mwa wakulima. Jambo la msingi ambalo limekuwa ni kikwazo kikubwa na mimi nitumie nafasi hii kuziagiza taasisi ambazo zipo chini ya Serikali jukumu la taasisi zilizoko chini ya Serikali siyo kuadhibu makampuni yanayochukua bidhaa kutoka kwa wakulima bali ni kuwasaidia ku-facilitate waweze kufanya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, utamaduni wa kuadhibu una-discourage investment na Serikali jana tumefanya maamuzi pamoja na Wizara ya Viwanda na Biashara kesi zote ambazo zinakabili kampuni Nne za tumbaku ambazo zilipigwa faini ya zaidi ya trilioni 11 kesi hizo ziondoke Mahakamani na tumewapa siku Saba na settlement agreement iwe imesainiwa ili wafanyabiashara hawa waweze kurudi kuendelea kufanya biashara. Ni azma ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais John Pombe Magufuli, kuhakikisha kwamba biashara inafanyika na mazingira yanakuwa sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili kampuni ya TLTC ambayo ameuliza Mama Sitta tumeanza maongezi na kampuni ya TLTC na tumefikia muafaka na nawashukuru sana TRA kwa hatua waliochukua crisis za VAT wameshakubaliana na settlement agreement imeshafikiwa na kesi imeshatoka Mahakamani. Wameahidi kuongea na Makao Kuu yao Universal ili waweze kuednelea na operation. Lakini watakapokuwa wao hawapo kampuni ya British American Tobacco mwaka huu inanunua tani 2,500 na itashiriki katika soko la kuanzia msimu wa 2019/2020. Kwa hiyo, wakulima hawatokuwa na matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.(Makofi)
MHE. RICHARD M. NDASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nami nimpongeze Hussein Bashe kwa majibu mazuri ya Serikali kwa zao la tumbaku. Tatizo lililoko kwenye zao la Tumbaku ni sawasawa kabisa na tatizo lililoko kwenye zao la Pamba. Mheshimiwa Waziri naelewa unajua tatizo ambalo limewakumba wakulima wa zao la pamba msimu huu, kwa sababu pamba mpaka sasa hivi bado iko kwenye maghala na majumba, Serikali ina utaratibu gani sasa wa kuwasaidia wakulima hawa wanaohangaika na pamba yao ili kusudi msimu ujao tatizo hili lisijitokeze tena? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli zao la pamba kumetokea mtikisiko katika soko la dunia na bei ya pamba katika soko la dunia imeshuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwezi Aprili ilikuwa ni Dollar 0.77 leo iko Dollar 0.60. Kwa hiyo bei imeshuka kwa senti 17 Dollar. Mpaka kufikia leo pamba iliyonunuliwa ni tani 265,000 pamba iliyobaki mikononi mwa wakulima ni tani 90,000. Serikali imechukua jitihada na intervention kupitia Benki Kuu kuweza kujaribu kuongea na mabenki yaweze kutoa fedha kwa makampuni yanayonunua pamba. Hatua ambazo tunachukua za muda mfupi ni hii intervention ya BOT kwa ajili ya kuhakikisha kwamba makampuni yanayoweza kununua pamba yaweze kupata fedha na yatakapokumbana na hasara Benki Kuu iweze kufanya intervention yasipate hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachukua hatua gani, tunapitia upya mfumo wetu wa ununuzi wa pamba, tutahakikisha Serikali ina-regulate kuhakikisha soko ndiyo linalo-determine bei ya kununua pamba na Serikali itasimamia kuhakikisha tunapunguza gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawaahidi wakulima wa pamba na Waheshimiwa Wabunge, matatizo yaliyojitokeza katika msimu huu katika mazao yote makuu ya kibiashara hayatojirudia katika msimu ujao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. (Makofi)
MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Serengeti pia tunalima tumbaku kama zao la biashara, kuanzia mwaka jana Alliance One kampuni ambayo imekuwa ikinunua zao hili toka kwa wakulima ilisitisha ununuzi wa tumbaku. Kwa hiyo, tuna tumbaku ya mwaka jana pia hii imepelekea wananchi kuacha kulima zao la tumbaku. Ningependa kufahamu ni lini sasa Serikali italeta mnunuzi kwa ajili ya wananchi wanaolima zao la tumbaku Serengeti ili wananchi waendelee kunufaika na zao hili?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, Alliance One ni moja kati ya kampuni ambayo iliamua kupunguza uwekezaji wake kwa sababu ya matatizo ya kesi yaliyokuwepo. Tarehe 12 wanakutana na Council ya Tobacco ili kuweza kufikia muafaka juu ya namna gani ya tumbaku zilizoko mikononi mwa wakulima zinanunuliwa zote. Kwa hiyo, tutai- consider kesi ya Serengeti kama special case na tutaifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho matatizo yanayokabili sekta ya tumbaku baada ya mwezi Oktoba matatizo haya yote yatakuwa yameamuliwa ndani ya Serikali na tutaamini kwamba wakulima wote wataendelea kufanya shughuli zao bila matatizo na hatuamini kwamba msimu ujao matatizo yaliyokuwepo yataendelea kuwepo katika sekta ya tumbaku. (Makofi)
MHE. ALFREDINA A. KAHIGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nakupongeza kwa majibu yako mazuri na kwa kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Kilimo. Mungu akutangulie. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali yangu mawili ya nyongeza, swali la kwanza; Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzuia wafugaji hao wasiweze kugonga ngozi mihuri ili wasikose soko la ngozi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wafugaji wanakamua maziwa mengi katika ranchi hizo na wafugaji wengine wa pembeni: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwatafutia vifaa vya kuweka maziwa yao? Maana vifaa wanavyovitumia siyo bora kwa kuwekea maziwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kuweka alama na kuchoma chapa ng’ombe, ni kweli kwamba inapunguza ubora wa mazao ya ngozi. Kuwepo kwa fursa ya uwepo wa maziwa mengi kutoka kwa wafugaji, nayo ni fursa ambayo ni lazima Serikali ichukue hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mifugo imeunda Kikosi Kazi ambacho kinahusisha Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Mifugo na Wizara ya Fedha na kikosi kazi hiki kinaanza kuzunguka kuangalia uwezekano wa namna gani ya kuanzisha maeneo madogo madogo ya usindikaji wa mazao ya mifugo, hasa maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kuweka alama, Wizara iko katika mchakato wa kuangalia ni namna gani tunaweza kutumia system ya tagging kwenye masikio ili kuweza kuweka numbering system na kuwatofautisha wafugaji. Hii itaondoa tatizo la kuweka michoro katika ngozi na kuongeza thamani ya ngozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake, lakini napongeza vile vile hatua zilizofikiwa za kufanya utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; pamoja na kwamba utafiti bado unaendelea, lakini tatizo la msingi tayari limepatikana kwamba kuna kiwango kidogo cha mboji, lakini pH vilevile ya udongo wa Ukerewe iko chini. Sasa swali langi, Wizara iko tayari kuijumuisha Ukerewe katika maeneo yanayopata ruzuku za pembejeo itakayoambatana na ushauri wa aina ya mazao yanayopaswa kulimwa kwenye maeneo yetu ya Ukerewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Ukerewe tuna fursa kubwa sana ya matunda, lakini tatizo kubwa, matunda yetu yamekuwa yanaharibika kwa kukosa soko. Tumejitahidi kupata wawekezaji kwa ajili ya kujenga viwanda, lakini tumekuwa tunakwama ama kutokana na kiwango cha malighafi inayozalishwa au aina ya matunda tunayoyazalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iko tayari kuwasaidia wananchi wa Ukerewe ambao wanalima matunda ili aina ya matunda yanayotakiwa iweze kulimwa, lakini sambamba na hilo, kusaidia kuwepo kwa kiwanda cha kusindika matunda haya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN MOHAMED BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mkundi kwa kazi kubwa anayofanya Jimboni kwake. Kuhusu suala la kupewa ruzuku kama ni special case, suala la ruzuku kwenye mbolea, hatuwezi kutoa commitment kama Serikali kwamba tutawapa watu wa Wilaya ya Ukerewe peke yao. Suala la ruzuku ama mabadiliko ya sera juu ya suala la kutoa ruzuku katika Sekta ya Kilimo, litatazamwa kwa ujumla wake kwa kuwa sasa hivi Wizara inapitia upya Sera yetu ya Kilimo ya Mwaka 2013 ili kuona mahitaji na namna gani tunaweza kutatua changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hatua za awali, tunaendelea kusisitiza wananchi wa Wilaya ya Ukerewe, watumie mbolea za minjingu na mbolea nyingine ambazo zinaweza kuongeza uzalishaji katika eneo lao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la matunda, siyo suala la Ukerewe peke yake, mazao yote ya horticulture sasa hivi kama Wizara tunafanya baseline study ya kuangalia ni namna gani tunaweza kufanya zoning ya kila eneo ili tuweze kutambua ni mazao gani ya high value yatokanayo na horticulture yanaweza kuzalishwa. Wizara sasa hivi iko katika hatua za awali kuangalia ni namna gani sekta ya horticulture inaweza kupewa kipaumbele na namna gani mazao ya matunda na mboga mboga yanaweza kupewa kipaumbele kama zao la muhimu kwa ajili ya export katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwaombe Waheshimiwa Wabunge watupe muda, kabla ya mwaka wa fedha ujao tuta-unveil Sera ya Wizara ambayo itafanya diversification katika sekta nzima ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuulizwa swali dogo la nyongeza. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri amekiri hapa kwamba mnafanya mapitio ya Sera ya Mbolea kwa ujumla, lakini kumekuwa na changamoto ya usambazaji wa mbolea na kutokufika kwa wakati kwenye maeneo husika na uhitaji wa uhalisia wa eneo husika.

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha usambazaji unafanyika kwa wakati na kwa mahitaji ya maeneo husika ili basi hizi ardhi zetu ambazo zimekosa rutuba ziweze kupata rutuba?
NAIBU WAZIRI KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba kuna upungufu katika baadhi ya maeneo katika suala la uasmbazaji wa mbolea na Wizara sasa hivi inachukua hatua ya kufanya reform katika Taasisi yetu ya TFC ili tuweze kuondokana na hili tatizo pale ambapo tunafanya bulk procurement kupitia TFC ili matatizo ya namna hiyo yasiweze kujirudia. Lakini yapo maeneo ambayo kuna wazalishaji wa ndani kama Minjingu ambao tumeamua kama Serikali kuwapa priority ili maeneo ya karibu ambayo kiwanda hichi kinafanya kazi na mbolea yake inaweza kutumika iweze kutumika kwa haraka, lakini sisi kama Wizara tunapitia mfumo mzima wa usambazaji wa pembejeo za mazao ili kuondoa mambo makubwa mawili:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ucheleweshaji, mbili wizi unaoendelea katika usambazaji wa pembejeo ambao siku ya mwisho anaenda kubeba mkulima. Kwa hiyo, tunaomba Waheshimiwa Wabunge kwamba mchakato huu unaendelea na tunaaamini kwamba msimu huu wa kilimo mambo mengi yatabadilika katika usambazaji wa pmebejeo. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi ya kuuliza swali dogo la nyongeza;

Mheshimiwa Mwenyekiti, msimu wa mwaka jana wa Pamba 2018/2019 tuliwaambia wakulima wa Pamba tuchange shilingi 100 kwa kila mkulima, iwe umekopa au hukukopa kwa maelezo kwamba msimu 2019/2020 hatukatwa pembejeo. Naomba kupata maelezo ya Serikali mwaka huu pembejeo wakulima wanakatwa au hawakatwi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwamba wakulima wanakatwa ama hawakatwi ni kwamba wakulima wanakatwa pembejeo za pamba msimu huu. Kilichotokea msimu uliopita fedha walizokatwa zililipa madeni ya pembejeo ambayo wakulima walipewa msimu uliotangulia, kwa hiyo msimu huu wakulima wa Pamba watakatwa pembejeo ambazo wamehudumiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezeee hapa na niseme na hili jambo liwe wazi, mfumo wa usambazaji pembejeo katika msimu ujao wa Pamba utabadilika. Tathmini ya awali iliyoonekana ni kwamba wakulima wa Pamba mwaka huu wanalipia pembejeo ambazo either hawakuzitumia ama wanabebeshwa mzigo, Wizara sasa hizi task force yetu iko kupitia mchakato mzima na tutachukua hatua kwa watu wote waliowaibia wakulima wa Pamba mwaka huu. Msimu ujao tunachokifanya mkulima wa Pamba Tanzania Cotton Board itatoa fomu ambayo itakuwa na duplicate ya fomu tatu, fomu moja ataachiwa mkulima aliyechukua pembejeo na itaonesha bei na thamani halisi, fomu nyingine itabaki kwenye AMCOS, fomu nyingine itabaki kwenye Ushirika ili msimu unapokuja wakati wa kuuza pamba gharama zake ziweze kuthibitishwa kabisa halali, kwa sababu sasa hivi kuna maeneo AMCOS na Ushirika unawaibia wakulima wa pamba ambao hawakuweza kubebeshwa gharama hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni kwamba wataendelea kulipa na tutabadilisha mfumo wa utoaji. (Makofi)
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa la wakulima wa Njombe ni udongo kuwa na tindikali nyingi zaidi na wataalaam wanajua hilo. Je, Serikali inatusaidiaje wakulima wa Njombe Mjini kutuletea chokaa ya kilimo ili kupunguza tindikali kwenye udongo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Wizara inafanya mobile sampling kwa nchi nzima kuangalia udongo na kuweza kuja na study ya wazi kujua kwamba wapi kuna tatizo gani na tuweze kupata solution. Tumuombe Waheshimiwa Wabunge watuvumilie wakati tunamaliza study hii tunaamini kufika mwisho wa siku huu tutakuwa na sample ya nchini nzima na kujua eneo gani linafaa kulima nini na eneo gani linahitaji mbolea gani ili tuweze kuwapitia huduma sahihi wakulima wetu badala ya kulima kwa kubahatisha. (Makofi)
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nianze kwa kumpongeza Naibu Waziri huyu kwa kuteuliwa. Nina swali dogo la nyongeza:

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kigoma haujafanyiwa soil profiling na Mkoa wa Kigoma una Chuo chake cha Kilimo cha Mbondo ni kwa nini sasa Serikali na hii tumeshaiomba huko nyuma, kwa nini sasa Chuo cha Mbondo kilichopo Kasulu kisifanywe ni Chuo Dada cha TARI kwa ajili ya profiling ya udongo katika Mkoa wa Kigoma, Mkoa ambao unapata mvua nyingi kuliko Mikoa mingine yote katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niseme kitu kimoja; tumetenga mwaka huu Shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuwekeza katika Chuo hicho kilichoko Kigoma, na specifically Kigoma itakuwa ni moja ya eneo la kimkakati la Wizara ya Kilimo kwa sababu ya Palm na tuna mpango wa UNIDO na FAO ambao tutawekeza fedha nyingi kwa ajili ya uzalishaji wa Palm Oil ili iwe ni solution ya kuondokana na kuagiza mafuta katika nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ombi ulilosema kwamba iwe ni Chuo sehemu ya TARI itakuwa chini ya TARI na itapewa hadhi kama vyuo vingine center za utafiti ambazo ziko chini ya TARI. (Makofi)
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri na nichukue nafasi hii kumpongeza pia Mheshimiwa Naibu Waziri kwa uteuzi alioupata na kwa kazi nzuri ambayo anaifanya toka ameteuliwa. Pamoja na hayo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ukiangalia majibu yanayoonyesha kwamba NARCO walipewa ramani tarehe 20 Oktoba, 1969, yanathibitisha ukweli kwamba vijiji vya maeneo hayo vilikuwepo kabla ya ranchi. Kwa kuwa tulipokuwa kwenye kikao na Mkuu wa Mkoa wa Kagera wa wakati huo na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, alioneshwa ramani ya NARCO ambayo ilionesha unapovuka Mto Kagera ukaenda mpaka wa Uganda hakuna kijiji, eneo lote ni la NARCO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne alishtuka na akaelekeza ramani hiyo siyo sahihi na akasema yeye alipokuwa askari alipigana vita na vijiji vilikuwepo na akaelekeza ramani hiyo irejeshwe kwake ili aweze kuipitia na ifutwe kwa sababu haitambui uwepo wa vijiji na toka wakati huo ramani hiyo imekuwa siri kubwa. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kunionesha nakala ya NARCO wanayoitumia kugawa maeneo hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali dogo la pili, pamoja na majibu mazuri kwamba hekta 21,571 zimetolewa lakini nakuwa na wasiwasi kwa sababu katika eneo hilo inaonekana kuna viongozi wanaolipwa ili wasione na kwa kuwa bado wapo maamuzi haya mazuri huenda yasilete tija. Je, yuko tayari kuniambia haya maeneo yaliyoongezwa ni yaleyale yaliyokuwa ya vijiji au ni maeneo yaliyokuwa ya NARCO sasa vijiji vimeongezewa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Dkt. Kamala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaozunguka mashamba ya NARCO katika Wilaya ya Misenyi wamekuwa na mgogoro na Serikali na NARCO kwa muda mrefu. Hatua zilizochukuliwa sasa ni kwamba mchakato wa kupitia upya mgongano wa ramani hizi umeshaanza katika ngazi ya wilaya na unaendelea katika ngazi ya mkoa. Wataalam kutoka TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi sasa hivi wameanza kupitia mipaka ili kuondoa tatizo hili la muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Balozi Dkt. Kamala achukue hatua tu kuwasilisha haya mawazo yake aliyoyasema na namna gani tunaweza kumaliza jambo hili kimaandishi Serikalini ili na yeye awe part ya mchakato huu wa kumaliza mgogoro wa mipaka katika vijiji hivi.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi ya maswali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri, nashukuru kwa majibu mazuri, lakini angalizo langu la kwanza naomba uwe makini na uende kwa kina zaidi kwani hicho kitengo cha kudhibiti panya hakiko sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Serikali kupitia Chuo cha Utafiti cha Sokoine, wamefanya utafiti njia mbadala ya kudhibiti hao panya kwamba wamegundua mkojo bandia wa paka unaoweza kuwadhibiti panya hao bila madhara makubwa kama tunavyotumia sumu ya kawaida. Swali langu, ni kwa namna gani Serikali kwa haraka inaweza ikasambaza matokeo ya utafiti huu, maana yake huo mkojo bandia wa paka huweza kukabiliana na adha hiyo ya panya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Hiyo hiyo Wilaya ya Malinyi takribani sasa ni mwaka wa tano tunasumbuliwa na ugonjwa wa virusi kwa ajili ya zao la mpunga, Kiingereza wanaita Rice Virus Disease ambapo kule kwetu jina maarufu Wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi tunaita Kimyanga; unashambulia mpunga, kipindi ambacho karibu unataka kuzaa unakuwa na rangi ya njano baadaye unaathiri kabisa uzalishaji. Sasa Serikali mna utaratibu gani kusaidia wananchi hawa wakabiliane na huo ugonjwa wa Kimyanga ambao ni adha kubwa sana kwa wakulima wa mpunga kwa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hili suala la Rice Virus Disease ambalo linaathiri Wilaya ya Malinyi, Wizara kupitia TARI, sasa hivi wataalam wetu wa TARI wanafanya special investigation kuweza kujua njia bora ya kuweza kudhibiti virus huyu asiweze kusambaa na hivi karibuni tutawasiliana na Mheshimiwa Mbunge na Halmashauri ya Mkoa wa Morogoro kwa ujumla ili kuweza kuwapa mbinu mbadala za kuweza kupambana na virus huyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili la Chuo cha Sokoine, kwa kuwa liko ndani ya docket yetu ya Wizara na sisi ni interested party, nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tunalichukua na tutalifanyia kazi. Hatua zozote ambazo zinaweza kutusaidia kupambana na changamoto ya panya, ingawa katika Mikoa ya Mtwara ni fursa kwao lakini tutahamasisha wenzetu wa Mtwara waje maeneo ya Malinyi kuweza kuwatega. Vilevile sisi kama Wizara tutashirikiana na SUA kuweza kutumia njia mbadala walioweza kugundua kuondoa hili tatizo.
MHE. AJALI R. AKBAR: Pamoja na Mheshimiwa kukupongeza wewe mwenyewe kwa kuchanguliwa kuwa Naibu Waziri, naomba unifikishie salamu zangu za dhati kwa Serikali kwa kupata hivi viuatilifu, lakini naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza ambayo ni madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, je, Serikali ina mpango gani juu ya bei ya korosho kwa msimu huu ambao umebaki kama miezi mitatu tu ili kuepuka mgogoro ambao ulikuwa umejitokeza mwaka jana ili bei ya korosho ibaki kati ya mkulima pamoja na mfanyabiashara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, kwa kuwa mwaka jana Halmashauri nyingi sana zilikuwa na madeni ambapo Halmashauri nyingi hazikupata ushuru. Je, Serikali itatoa waraka sasa wa asilimia tano ya farm gate price kama Sheria inavyosema kuliko kutoa ile bei elekezi ile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atoe waraka kama Sheria inavyosema kwamba tupate asilimia tano na usitoe ile asilimia elekezi ili tupate kulipa madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la msimu ujao wa korosho, kwanza Serikali katika msimu ujao wa korosho tumeamua na wiki ijayo Waziri wa Kilimo atatangaza hadharani utaratibu na namna gani ya mfumo wa ununuzi wa korosho utakavyokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa ununuzi wa korosho katika msimu ujao utakuwa ni mfumo wa wafanyabiashara kununua zao la korosho na Serikali itakuwa pale kwa ajili ya kuangalia utaratibu ule haumwathiri mkulima. Vilevile Serikali itatangaza utaratibu wa ku-bid kwa wazi. Hatutatumia utaratibu wa viboksi na usiku wa manane watu wa kwenda kutengeneza cartel ambayo siku ya mwisho inakwenda kutuletea matatizo. Transparency ndiyo itakuwa msingi wa ununuzi wa korosho katika msimu ujao na hatutarudi nyuma na yale matatizo yaliyojitokeza hayatajitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekitiu, kuhusu farm gate rate, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge, hatutaongeza rate ya ushuru wa cess kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anafikiria ufanyike, kwa sababu utaongeza gharama za off takers na siku ya mwisho tunavyoongeza ushuru ambao mfanyabiashara anaulipa, siku ya mwisho anayekwenda kuumia na kupata bei ndogo ni mkulima. Kwa hiyo, hatuwezi kuongeza gharama katika biashara. Jukumu la Serikali ni kupunguza gharama katika kufanya biashara ili wafanyabiashara na wakulima waweze kupata faida. (Makofi)
MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya serikali; hata hivi nitakuwa na swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya changamoto kubwa ambayo inavikabili vyama cha ushirikia kwa maana AMCOS wilayani Mbinga ni nikukosa mitaji kwa ajili ya undeshaji washughuli zake, jambo ambalo linasabisha kukopa kutoka kwenye benki za biashara kwa riba kubwa.

Je, serikali ina mpango gani wa kufungua tawi la Benki ya Kilimo Wilayani Mbinga ili kuziwezesha AMCOS hizo kukopa kwa riba naafuu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Msuha kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba vyama vingi vya ushirika ama watanzania wengi walioko sekta ya kilimo walioko vijijini wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa mitaji na hasa pale ambapo wamekuwa wakikopa katika benki za biashara. Serikali iliaangiza Tanzania Agriculture Development Bank kuingia akubaliano na benki za bishara kama NMB na CRDB; na benki zote hizi sasa hivi zina mahusiano ya moja kwa moja na Benki ya Kilimo. Umetengenezwa utaratibu ambapo mwananchi ama taasisi yoyote ambayo inajihusisha na kilimo iliyoko wilayani inaweza kwenda katika dawati lililopo katika NMB ama CRDB ambalo linaiwakisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, Benki ya Maendeleo ya Kilimo ni benki ambayo kimkakati hawezi kwenda kufungua matawi nchi nzima katika kila wilaya kwa sababu ya namna ambavyo imeundwa. Ni benki ya kimkakati ambayo ni ya uwekezaji wa muda mrefu katika sekta ya kilimo na haifanyi commercial activities. Kwa hiyo ningemshauri Mheshimiwa Mbunge awahamasishe vyama vyake vya msingi vya ushirika viende katika Benki za NMB ama CRDB zilizopo katika wilaya zetu ambazo zitayari zina madawati ya mahusiano ya kibiashara na Benki ya Maendeleo ya Kilimo, na huko watapata huduma wanazohitaji za muda mrefu.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, naishukuru serikali kwa majibu mazuri, lakini pia naipongeza kwa kurejesha mali za ushirika mikononi kwa washirika wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu. Kwa kuwa elimu ya ushirika ni elimu ambayo inahitajika sana kwa wananchi na hasa tukizingatia ambavyo ushirika nchi hii umekuwa ukipata misukosuko hadi umefikia kutoka kwenye wizara mpaka hadi kwenda idara; na kwa kuwa nchi hii ina bahati sana kuwa na Chuo Kikuu cha Ushirikia pale Moshi, na wote washirika wanatakiwa kupata elimu.

Ni lini sasa serikali italeta muswada Bungeni kubadili mafunzo kwa wote wale ambao wanashiriki ushirika waende kwenye chuo kile kusomeshwa na kuelewa ushirika nini kama alivyoeleza Naibu Waziri?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya elimu ya ushirika miongoni mwa viongozi wa ushirika vilevile na wanachama wa vyama vya ushikirika. Wakati tunapitia, na tutakapoleta sheria ambayo tunatarajia kuileta katika Bunge lango Tukufu. Wizara ya kilimo sasa hivi imeamua kuanzisha mkakati wa kutoa elimu ya ushirika kwa kukihusisha Chuo cha Ushirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi uliopita tumeanza na vyama vikuu vya ushirika, viongozi wote walikuwa hapa Dodoma, na sasa hivi watalaamu kutoka Chuo cha Ushirika Moshi wamekatiwa zones kwenda kutoa elimu katika vyama vya msingi vilivyopo katika wilaya zetu na mikoa yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na nitumie nafasi hii kusisitiza ofisi za serikali za wilaya na mikoa zitoe ushirikiano kwa Warajis wa Mikoa na walimu walioletwa katika mikoa kwa ajili ya kutoa elimu kwa vyama vikuu na vya msingi vilivyopo katika wilaya zetu. Tumewekeana deadline kufika mwezi wa Aprili wataalamu hawa waliogawana katika zones sita watakuwa wamefika katika wilaya zote na mikoa yote kuanza kutoa elimu ya ushirika kwa viongozi wa vyama vya msingi vya ushirika.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa Mikoa ambayo imekuwa ikijishughulisha na kilimo cha chakula na biashara na kwa kufanya hivyo, wakulima wengi wanahitaji kupata mbolea kwa ukaribu.

Pamoja na maelezo mazuri ambayo yametolewa na Naibu Waziri, naomba Serikali ione sasa wakati umefika wa kuondoa hizo tozo zote kwa hao wafanyabiashara ambao watakuwa wamekidhi vigezo ili kuwaruhusu sasa waende wakafungue maduka huko vijijini ambako ndiko waliko wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na malalamiko kwa baadhi ya Mawakala ambao siyo waaminifu, wamekuwa wakiuza mbolea kinyume na bei elekezi na hii inapelekea kuwafanya wakulima wetu kununua mbolea na pembejeo kwa gharama ya juu sana. Je, Serikali inakuja na kauli gani kwa Mawakala ambao wamekuwa wakiongeza bei za pembejeo?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chikambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la tozo, Wizara ya Kilimo sasa hivi inapitia upya tozo na gharama mbalimbali ambazo zinaweza kupunguza na kurahisisha shughuli za biashara katika sekta ya kilimo. Kwa kuwa Serikali inakuja na Blue print nataka nimuombe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwa ujumla, huo utakuwa ni wakati mzuri sana wakati tunafanya mapitio ya Sheria ya Kurahisisha Mazingira ya Kufanya Biashara kuweza sote kushauriana na kuja na mwelekeo sahihi. Hata hivyo, katika mwaka wa fedha unaokuja, zipo baadhi ya tozo ambazo tutazileta Bungeni kwa ajili ya kuomba namna ya kuweza kuzibadilisha na kurahisisha mazingira ya kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la wafanyabiashara wasio waaminifu, nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza sana Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma kwa hatua alizochukua za kupita katika maduka na kuwakamata wafanyabiashara ambao wanakwenda kinyume na maelekezo ya Serikali. Kumekuwa na tatizo la wafanyabiashara wa viuatilifu na mbolea, kuhusu suala la bei elekezi, tumeagiza kwamba yeyote anayekwenda kinyume na maelekezo ya Serikali katika kuuza mbolea tofauti na bei elekezi, viongozi walioko katika ngazi za Wilaya na Mikoa waweze kuwakamata na kuwachukulia hatua na kuwapeleka katika vyombo vya Sheria kwa sababu hiyo itakuwa ni dhuluma na wizi kwa wakulima na ni jambo ambalo kama Serikali hatuwezi kuliruhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo, tunaendelea kusisitiza wafanyabiashara wote walioko katika sekta ya kilimo wanaouza mbolea na pembejeo na mbegu ambao wamekuwa siyo waaminifu kwa kuuza mbegu feki, kwa kutoa viuatilifu feki, Serikali inafuatilia kwa karibu. Tunatumia nafasi kuwaomba Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kuhakikisha wanakagua na nawataka wananchi wanaponunua wahakikishe wanaomba risiti ili watakapokutana na tatizo iwe rahisi sisi Serikali kuweza kuchukua hatua na kuwafuatilia na kuwapeleka katika vyombo vya sheria.
MHE. MARY P. CHATANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wakulima wanapata adha hii kubwa ya kununua mbolea kwa bei kubwa, kwa nini Serikali sasa isianzishe maduka haya ya pembejeo huko vijijini kupitia Mawakala ili kuwaletea unafuu wakulima kwa ajili ya ununuzi wa mbolea?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mama Chatanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali haifanyi biashara, tuna encourage private sector kufanya biashara na kuwekeza na kuhakikisha kwamba wanafika maeneo ya wakulima vijijini. Jukumu letu ni kujenga mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeanzisha mfumo wa Bulk Procurement ili ununzi uwe wa pamoja kupunguza gharama. Tunaendelea kuuangalia mfumo huo kwa sababu katika soko la dunia kuna nyakati ambazo bei ya mbolea inakuwa juu na kuna nyakati ambazo inakuwa chini. Tunachokifanya sasa hivi ni kuangalia ni nyakati gani ambazo bei ya mbolea inakuwa chini ili tiuweze kuutumia mfumo wa Bulk Procurement wafanyabiashara waweze kununua wakati huo, mtaona mwaka hadi mwaka bei za mbolea zimekuwa zikishuka. Hata sisi tunaamini kwamba bado bei hizi hazijashuka kiwango kinachostahili lakini tunaendelea kufanya jitihada hizo na kwa mfumo wa Bulk Procurement ndiyo itakuwa njia sahihi ya kuweza kuhakikisha kwamba wakulima wanapata mbolea bora na kwa bei nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu biashara, hatutafungua maduka ya Serikali vijijini bali ni kuhamasisha sekta binafsi na kuwajengea mazingira ili kupunguza gharama na kupunguza utitiri wa regulatory bodies ili wafanyabiashara waweze kwenda kufungua maduka haya vijijini na kuwapatia huduma wakulima. Dhumuni la Serikali ni kuwawezesha wafanyabiashara na Watanzania waweze kufanya biashara na wala siyo Serikali kufanya biashara katika eneo hilo. Tuta-intervene pale ambapo kuna jambo la muhimu kufanya namna hiyo.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo yatakuwa na afya katika Ushirika wetu. Hata hivyo, bado kuna upungufu kwenye kaguzi zinazofanywa katika Vyama vya Ushirika. Mkaguzi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) anakagua na ripoti yake inapelekwa kwa Vyama vya Ushirika hivyo kuwepo kwa mgongano wa maslahi. Je, Serikali haioni ni muda muafaka Vyama Vikuu vya Ushirika vikakaguliwa na Mkaguzi wa Mkuu wa Hesabu za Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Chama cha Ushirika Nyanza, SHIRECU na SIMCU vina mali nyingi na Serikali inafanya juhudi ya kutoa fedha kwa ajili ya ukarabati wa vinu vya kuchambulia pamba. Nimeshudia Naibu Waziri akifanya ukaguzi wa vinu hivyo kujiridhisha na kuona hali halisi. Hata hivyo, tukumbuke katika maeneo hayohayo kuna vinu vya kuchambulia pamba vinavyomilikiwa na watu binafsi wanaofanya biashara kwa faida hivyo kuwepo na ushindani. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Vyama vya Ushirika vinajisimamia na kuwa endelevu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Komanya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama Serikali nikiri kumekuwa na udhaifu katika mfumo wa Ushirika na ndiyo maana Serikali imeamua kufanya mapitio makubwa ya Sera pamoja na Sheria ya Vyama vya Ushirika. Kama alivyosema kuhusu suala la COASCO na kushauri kwamba CAG akague Vyama Vikuu vya Ushirika; kwa mujibu wa sheria, CAG anakagua fedha za umma zinazopitishwa na Bunge, Vyama vya Ushirika ni private entity kwa muundo wake, ni vyama vya hiari.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, katika mapendekezo tunayokuja nayo ili kuifanya COASCO iwe na taasisi nyingine inayoifanyia oversight, bado ndani ya Serikali tunaangalia ni namna gani tutaifanya COASCO iweze kufikia malengo tuliyonayo ya kuweza kusimamia Vyama vya Ushirika na kuwa na nguvu ambayo tunaitarajia. Ni kweli sasa hivi wakifanya ukaguzi, taarifa pamoja na kuipeleka kwa Mrajisi lakini vilevile wanaipeleka kwa wanachama husika wa Chama cha Ushirika. Hii imekuwa ikileta matatizo na pale ambapo kunakuwa na viongozi wasiokuwa waaminifu huweza kutumia nafasi hiyo vibaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwa sasa COASCO wanafanya kazi nzuri, kwa miaka hii miwili wame-produce report ambayo imeweza kutuonyesha taswira ya Vyama vyetu vya Ushirika vina hali gani na sisi kama Wizara tumeanza kuchukua hatua. Kutokana na report hiyo, tumeona upungufu ambao unatulazimu sisi kama Serikali kuja na mabadiliko katika muundo wa Ushirika na namna ambavyo COASCO itafanya kazi na pale ambapo tunaamini kwamba kuna umuhimu wa kumuingiza CAG hatutasita kuchukua hatua hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Nyanza, SIMCU na SHIRECU; moja, ni sahihi kwamba ginnery nyingi na miradi mingi iliyokuwa chini ya Ushirika imefeli. Nini tunafanya kama Serikali? Tumepitia ginnery zaidi ya nane na tumeshazifanyia feasibility study ili kuweza kuziinua zikiwemo ginnery za Chato, Mbogwe, Kahama (KACU), Lugola na Manawa. Ginnery hizi tumezipitia na kuziangalia kama zinaweza kuanza kufanya biashara. Taarifa hii imeshakamilika, tunaifanyia kazi tukishirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini muundo wa uendeshaji tumesema clearly kwamba ginnery hazitaendeshwa na Wenyeviti wa Vyama vya Ushirika. Ginnery zitakuwa ni business entity zinatazoendeshwa na professional people ambao watazisimamia kibiashara ili ziendeshwe kibiashara. Mara nyingi tumekuwa tukitoa mifano, Kampouni kama Vodacom, Airtel na multi-nation zingine, shareholders hawaendeshi wana contract management na hiyo ndiyo model tutakayotumia kuendesha ginnery hizi ili ziweze kujiendesha kibiashara, hatutaziendesha kama taasisi za huduma.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naomba niipongeze Serikali kwa juhudi kubwa ambazo imefanya kwa kurejesha Vyama vya Ushirika. Hata hivyo, kumekuwa na malalamiko mengi sana kuhusu vyama hivi na matatizo yake ni mengi. Wakulima wanapokuwa wamepeleka mazao yao mara nyingine hawalipwi kwa wakati au fedha zao kupotea kabisa. Sasa nataka kuiuliza Serikali, je, itakuwa tayari yenyewe kama Serikali kuweza kufidia pale ambapo Vyama vya Ushirika vimeshindwa kuwalipa wakulima hawa fedha zao kwa wakati ama kuwafanya wakulima wapate bima zao za mazao ambazo zinakuwa ni kwa ajili ya majanga mbalimbali kama mafuriko, nzige, ukame na kadhalika, pamoja na kutokulipwa iwe ni kama janga mojawapo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Martha Mlata, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu suala la bima; wakati wa Nane Nane Serikali ilizindua Bima ya Mazao. Nitumie nafasi hii kuwahamasisha wakulima kuhakikisha kwamba wanajikatia insurance za mazao yao. Pamoja na hatua hiyo kama Serikali na Wizara tumeanza kupitia gharama za bima ya mazao na hivi karibuni tutakutana na insurance companies ambazo zinatoa bima katika sekta ya kilimo ili tuweze kukubaliana nao na kutengeneza road map itakayo-guide suala la insurance. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Ushirika, napenda tena kurudia kusema ndani ya Bunge hili Tukufu. Ushirika haununui mazao, wao ni conduit ya kumkutanisha mkulima na mnunuzi. Tunatumia Ushirika kama sehemu ambayo wakulima wadogo wadogo watapeleka mazao yao na watakuwa na bargaining power juu ya hatima ya mazao yao. Vilevile niseme pale ambapo Chama cha Ushirika kitashiriki katika ubadhirifu wa kumuibia mkulima, tutawachukulia hatua stahiki na kali kama ambavyo tumekuwa tukifanya. Navyoongea sasa hivi viongozi wa ushirika sehemu mbalimbali ambao wamekula fedha za wakulima wako magerezani na wamechukuliwa hatua na kupelekwa kwenye kesi za uhujumu uchumi. Hivi karibuni tumewaweka ndani viongozi wa Chama cha Chai cha MVYULU kilichopo Wilaya ya Lupemba ambao walikuwa wamejibinafsishia mali za wakulima ziwepo magari, mashamba na nyumba na tutaendelea kufanya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaeleze Watanzania na Waheshimiwa Wabunge hatuwezi kukimbia changamoto. Ubadhirifu ulikuwepo hatuwezi kuua mfumo mzuri wa sekta ya kilimo kwa sababu ya viongozi wabadhirifu. Sisi kama Wizara tutasimamia kuhakikisha kwamba ushirika unakuwa safi na kuweza kufikia malengo ya Serikali. (Makofi)
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji naomba nijikite kwenye suala la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kuhusiana na suala la pamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli mnyororo wa thamani katika suala la pamba cotton to cloth unapaswa kufanyiwa mkakati mahsusi kwa kumwezesha mkulima aweze kupata thamani ya kile anachokifanya, lakini swali langu ni kwamba wakulima wa pamba ambao mwaka hadi mwaka wamekuwa wakifanya kazi ya kulima pamba wanakuwa wanapata hasara; kwa mfano leo hii wakulima wa Mkoa wa Simiyu na hasa Wilaya ya Busega wameuza pamba toka mwezi wa Tano mpaka leo hawajalipwa fedha yao? Sasa Mheshimiwa Waziri haoni kwamba hii ni ku-discourage wakulima wasiweze kufanya kilimo kizuri zaidi na nini tamko la Serikali juu ya hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Raphael Chegeni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba baadhi ya wakulima wa pamba hawajalipwa fedha zao, pamba mwaka huu mpaka sasa hivi jumla ya bilioni mia nne kumi na saba zimeshalipwa kwa wakulima wa nchi nzima. Wakulima ambao hawajalipwa wanadai bilioni hamsini kufikia sasa hivi na sababu ya msingi ni nini? Ni kwa sababu lazima tufahamu kwamba pamba asilimia zaidi ya 80 inakwenda nje ya nchi, wanunuzi wetu wanakabiliwa na mtikisiko wa bei ambao umewakabili katika soko la dunia na sisi kama nchi tulitoa maelekezo ya bei ya kununulia kama Serikali. Haya yalikuwa maamuzi ya Serikali kwa ajili ya kumlinda mkulima asipate hasara, lakini Serikali imefanya intervention kuongea na financial institutions zote na kuweza kuwasaidia namna gani ya kupunguza interests kwa wanunuzi ili waweze kwenda sokoni kununua bei ya pamba kwa Sh.1,200.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, siku ya tarehe 14 tutakutana na Kamati ya wanunuzi wote makampuni yote yanayonunua ili kuangalia flow ya fedha inavyokwenda, lakini pamba yote iliyokuwa kwa wakulima imeshakusanywa, sasa hivi kilichobaki mkononi mwao ni tani 5,000 tu, ambayo tunaamini mpaka mwisho wa mwezi huu itakuwa imekwishaondoka mikononi mwa wakulima na msimu unapoanza tarehe 15 tunaamini wakulima wote pamba yao itakuwa imeondoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili la intervention ya bei Serikali tunajitahidi kupunguza gharama kuanzia msimu huu unaokuja na hatutoingilia kupanga bei, bei itakuwa determined na soko na sisi jukumu letu kama Serikali itakuwa kuhakikisha mkulima hatopata hasara. Tutatafuta njia zingine za kumlinda mkulima kuliko kumwathiri mnunuzi. Hii ndiyo hatua ambayo tunachukua kama Serikali. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kabla sijauliza maswali ya nyongeza, niruhusu niendelee kuwapa pole wananchi wa Jimbo langu la Korogwe Vijijini na Mkoa mzima wa Tanga kwa mafuriko makubwa yaliyotupata siku chache zilizopita. Tunaendelea kutumaini juhudi ya Serikali kurejesha miundombinu yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; moja ya sababu ya nchi tunazoshindana nazo kwenye soko la mazao ya viungo na mazao ya bustani kufanya vizuri ni wao kuwa na mamlaka za kusimamia mazao haya. Je, ni lini Serikali yetu itaona umuhimu wa kuanzisha Mamlaka ya Kusimamia Mazao ya Viungo na Mazao ya Biashara?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; wananchi wa Tarafa ya Bungu, Wilaya ya Korogwe, ni wakulima wakubwa na wazuri sana wa mazao ya viungo na zao la chai, lakini tumekuwa na changamoto kubwa sana ya bei kwenye zao la chai. Je, ni upi mkakati mahususi wa Serikali wa kuhakikisha kwamba wanaboresha bei ya zao la chai ili kuweza kuwaletea tija wananchi na wakulima wa zao la chai nchini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mnzava kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kutumia nafasi hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge pamoja na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba Wizara ya Kilimo inafahamu umuhimu wa kuanzishwa kwa taasisi itakayosimamia mazao ya horticulture na mazao ya viungo. Hivi sasa tunapitia mfumo na muundo wa Wizara kupunguza idadi ya bodi na kuanzisha mamlaka chache ambazo hazitazidi tatu, mojawapo ikiwa ni Mamlaka ya Maendeleo ya Mazao ya Horticulture.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwenyezi Mungu akijaalia hivi karibuni Bunge hili litapokea sheria ambayo itaonesha mabadiliko ya muundo wa taasisi mbalimbali ndani ya Wizara ya Kilimo ili kuipa sekta hii nafasi inayostahili kwa sababu ni subsector ndogo katika Sekta ya Kilimo inayokua kwa kiwango kikubwa sana na inahitaji attention inayostahili. Kwa hiyo nimtoe hofu kwamba tuko katika hatua za awali na kabla ya kufika Bunge lijalo la Bajeti tutakuwa tumeshaanzisha Mamlaka ya Mazao ya Horticulture.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la chai; ni kweli kama Serikali hatua tunazochukua mojawapo sasa hivi tuko katika hatua za mwisho za kuanzisha a primary market katika eneo la Dar es Salaam ili tuwe na mnada wa kwetu hapa Tanzania. Tumesha-earmark eneo na sasa hivi tuko katika hatua za awali kutengeneza utaratibu ili chai yetu badala ya kwenda kuuziwa katika soko la Mombasa sasa ianze kuuziwa katika soko la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tutatumia mfumo wa TMX ili kuwaruhusu wanunuzi duniani waweze ku-bid. Mchakato huu unawahusisha Sekta Binafsi ambao wamewekeza katika chai ili kuhakikisha kwamba zao la chai linapata soko na bei ya uhakika. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge tunaamini kwamba ndani ya muda mfupi tutaanzisha soko la kwetu ndani ya Tanzania na chai yetu itauziwa hapa na itapunguza gharama na kumpatia mkulima bei nzuri.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Katika Mkoa wa Simiyu tayari mbegu za pamba zimeshaanza kusambazwa na kupata mbegu za pamba kwa wakulima mpaka uzinunue. Wapo baadhi ya wakulima bado hawajalipwa pamba na wanunuzi; je, Serikali inawasaidiaje ili wakulima hao waweze kupata mbegu za pamba?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua tatizo hilo alilolisema Mheshimiwa Leah Komanya, ni kweli kampuni binafsi na ningeomba kupitia Bunge Watanzania wote wakaelewa; walionunua pamba sio Serikali ya Jamhuri ya Muungano, walionunua pamba ni kampuni binafsi za Watanzania, lakini tunafahamu kwamba Watanzania wote hawajalipwa wanaodai kampuni hizi. Mpaka sasa wameshalipa bilioni 417, wakulima wanadai bilioni 50. Tarehe 14 tutakutana na wanunuzi ili kulitatua tatizo la wao kumalizia kulipa kwa wakulima ili wakulima waweze kupata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo vilevile makampuni yaliyopewa haki ya kusambaza mbegu bora katika maeneo ya wakulima wa pamba nao tutakutana nao ili kutengeneza utaratibu ambao hautowalazimisha wakulima wanaodai kulazimishwa kulipia mbegu ya pamba. Tutatengeneza utaratibu ambao utamfanya mkulima kama anaidai kampuni kampuni hiyo impe mbegu wakati anamlipa atakata gharama yake ya mbegu alizompatia. Kwa hiyo tarehe 14 tutamaliza tatizo hili na hili halitakuwa tatizo tena muda mfupi ujao.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Zao la pilipili manga na viungo vingine kama hiliki na mdalasini ni mazao ambayo tunayategemea sana katika Wilaya ya Muheza, lakini wakati wa msimu wa mazao haya ya viungo panakuwa na vurugu kubwa sana Muheza hususan ya wanunuzi wa mazao haya kiasi kwamba inaelekea kushusha bei sana za viungo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango gani kuweza kuwasaidia Wana-Muheza ili kuhakikisha kwamba inaweka maghala na kuingia kwenye utaratibu wa uuzaji wa viungo hivi kwa njia ya mnada? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; pamoja na zao hili, lakini hakuna utaratibu wa ku-add value kwenye mazao haya ya viungo; nilitaka kujua Serikali ina mpango gani wa kujaribu kuwasaidia Wana-Muheza kwa ajili ya kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya kuchakata viungo hivi ili kuviongezea thamani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mpango wa Wizara ya Kilimo sasa hivi kuhakikisha kwamba tunabadilisha mfumo wa uuzaji na wanamasoko wa mazao ya kilimo kwa ujumla wake. Moja ya mkakati tulionao kama Wizara ni kuhakikisha tunafanya mfumo wa kuweko maghala na kuleta minada katika maeneo mbalimbali na mkakati huu utahusisha siyo tu mazao ya pilipili manga kama ambayo amesema Mheshimiwa Adadi, lakini vilevile tutaangalia mfumo wa uuzaji wa mazao yote hata haya tunayoita ya mkakati ikiwemo pamba kama ambavyo tumeanza kwenye chai kuhakikisha kwamba tunaanzisha soko katika Jiji la Dar es Salaam la kuuzia chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatuma wataalam kuangalia mambo mawili; moja, viability ya kuanzisha mfumo wa stakabadhi ghalani katika eneo la Muheza kama halitoathiri bei iliyoko sasa hivi. Kwa sababu tunaweza kwenda kuanzisha mfumo ambao ukapelekea kuangusha bei ya zao. Kama uuzaji wa kutumia stakabadhi ghalani utamwongezea mkulima bei nzuri, tutaufanya huo na tutatuma wataalam waende wakafanye tathmini ili tuweze kuanzisha Warehouse System Receipt kwa eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu value addition, nitumie nafasi hii nimwombe Mheshimiwa Mbunge wa Muhesza, kama anaweza kuwaweka wakulima wake katika makundi na uzalishaji wao ukawekwa katika makundi ya pamoja na kutengeneza vyama vya wakulima wadogo wadogo wa pilipili manga na mazao mengine katika eneo hilo, Serikali iko tayari kuwashika mkono kupitia njia mbalimbali za kuweza kuwapatia funding ili waweze kuanzisha process ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine, katika Halmashauri zetu tunakusanya fedha za cess ni lazima tutengeneze mipango ya kutumia fedha zinazotokana na mazao ya kilimo ziweze kurudi kuongeza thamani na kuwasaidia wakulima kufaidika na kodi zinazokusanywa na mazao haya ili angali zile 10% za Halmashauri, basi tuweze kuwakopesha wakulima wadogo wadogo waweze kuanzisha small process industry na pale ambapo wanahitaji msaada wa Serikali Kuu, sisi kama Wizara ya Kilimo tuko tayari kuwashika mkono. (Makofi)
MHE. DKT. GODWIN A. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wizara ya Kilimo imefanya kazi kubwa sana kwenye maeneo ya kufufua haya mazao ya mkakati lakini vilevile kushughulikia Vyama vya Ushirika. Katika Mkoa wa Kilimanjaro vile vile kazi kubwa imefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuomba, ukienda Wilaya ya Siha Vyama vya Ushirika vingi vina matatizo. Kwa mfano, ukienda Sanya Juu utakuta wanachama 1,800 wameibiwa, SACCOS yao imekufa na fedha zimepotea, lakini ukienda kwenye mashamba yote yaliyoko Wizara ya Siha, ukienda Kashashi kuna ushirika wenye shida. Kwa hiyo, utaona kuna matatizo ya ardhi lakini kuna suala zima la kufufua zao la kahawa.

Mheshimiwa Waziri nilikuja ofisi kwako kukuomba twende Wilaya ya Siha na upate siku isiyozidi mbili za kutosha kwa ajili ya kuangalia matatizo yote haya. Sasa ni lini sasa utaweza kuja hapo ili ushirikiane na Comrade Ndaki Stephano Muhula, Mkurugenzi mzuri sana wa Wilaya ya Siha ili tuweze kufikia muafaka mzuri wa kufufua ushirika kwenye Wilaya ya Siha?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Dkt. Mollel kwamba lini niko tayari kwenda? Tukimaliza Bunge hili mimi na yeye tukae, tupange ratiba, tuweze kwenda Hai pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ushirika na ubadhirifu unaoendelea Kilimanjaro, nataka tu nimhakikishie kwamba kuna timu yetu inaendelea na kufanya tathmini na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba yeyote atakayekuwa ameshiriki kula fedha za Ushirika, awe ndani ya Serikali au kwenye Vyama vya Ushirika, tutawachukulia hatua.
MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafahamu kwamba zao la mbaazi lilipata soko hivi karibuni kidogo ilipanda kutoka shilingi 150/= ya mwaka jana mpaka shilingi 900/=, lakini imeanza ku-drop. Tatizo kubwa ni kwamba msimu wetu unapokuwa unaanza, wale ambao wanatupa soko kama India, Pakistan, na nchi nyingine wao kule msimu ukianza huku kwetu zao hilo linakuwa haliuziki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nifahamu sasa mkakati wa Serikali kusaidia wananchi wetu ili waendane na msimu wa nchi ambazo wanatumia zao hili kwa sababu hatuna soko la ndani sisi wenyewe.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba inapofika baada ya Oktoba bei ya mbaazi huanza kushuka na sababu moja, unakuta kwamba quarter yetu inakuwa imekaribia kwisha wakati nchi nyingine zimeanza kuzalisha. Kwa hiyo, kama Wizara ya Kilimo, tunachokifanya cha kwanza ni kujaribu kuwahamasisha wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nitumie nafasi hii kuendelea kuwahamasisha wafanyabiashara na hasa wanaonunua mazao ya mbaazi. Katika kipindi cha Septemba na Agosti, kipindi hiki bei ya mbaazi na demand yake inakuwa ni kubwa. Niwashauri kwamba, ni kipindi cha kutoa stock na kuuza kabla ya production ya upande mwingine haijaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, sisi kama Wizara tunafanya jitihada kuongea na masoko kama ya India ili kuongeza quarter na volume ambayo tunahitaji. Yapo mazao ambayo mpaka sasa hatuko tayari kuyaingiza katika mfumo wa Stakabadhi Ghalani likiwemo mbaazi ili kuruhusu free trade iweze kuchukua nafasi yake na kwa sababu kuna sensitivity ya bigger consumer wa dunia vilevile ndio wazalishaji wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapunguza bureaucracy kuruhusu watu waendelee kufanya hii biashara. Pia Wizara tunaendelea kufanya jitihada kuongeza quarter ya ku-export mbaazi, lakini nasisitiza mwezi wa Nane na wa Tisa tunapata bei nzuri, wakulima na wafabiashara wanaouza mbaazi hakikisheni mnauza mbaazi hizo wakati ambapo bei imefika juu. Ilifika mpaka shilingi 900/= na kuna maeneo ilifika mpaka shilingi 1,000/=. Mkiendelea ku-hold stock, Oktoba na Novemba tunaelekea duniani ambao wanazalisha na wenyewe wanakuwa wameingiza sokoni. Kwa hiyo, competition inakuwa kubwa na bei inaanguka.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi kwa niaba ya wananchi wa Urambo, niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika jibu lake imekiri kwamba ilikuwa na kikao na hawa wanunuzi wa tumbaku wanaotaka kuondoka nchini:-

Je, Serikali inaweza kutuambia kwamba baada ya mazungumzo haya ya mwezi wa Tisa imefikia muafaka gani ili kampuni hizi ambazo zilikuwa zinanunua tumbaku nyingi hasa Urambo na Tabora kwa ujumla waendelee kununua tumbaku na pia kulinda ajira ya wale waliokuwa wakifanya kazi katika kampuni hizo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanaotishia kuondoka, kama kweli hawatakubaliana na Serikali waondoke, Serikali itafanya nini kuhusu viwanda ambavyo walikuwa wamenunua kama kile cha Morogoro na pia magodauni mengi ambayo walikuwa wamenunua sehemu nyingi sana kule ambapo wananunua tumbaku? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza siyo dhamira ya Serikali kuona kwamba kuna mwekezaji yeyote ambaye amewekeza anaondoka nchini. Kwa hiyo, dhamira yetu ni kuendelea kufanya maongezi nao; na kufuatia maongezi tuliyofanya mwezi Septemba, kampuni tatu za tumbaku zilirudi kununua tumbaku ambayo ni maarufu kwa jina la makinikia ambayo ni un-contracted tobacco. Wameenda kununua jumla ya kilo milioni saba kati ya kilo milioni 12 ambazo zilikuwa zimebaki mikononi mwa wakulima. Kwa hiyo, tunaendelea kuongea na makampuni haya ili yaweze kuendelea kununua tumbaku na kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kampuni ambayo imeonesha nia ya kuondoka na kufunga shughuli zake, Kampuni ya TLTC; hoja za TLTC zilikuwa ni tatu. Moja, ni suala la kesi iliyokuwepo kati yake na Manispaa ya Morogoro. Tumefanya kikao mwezi wa Kumi katika Mji wa Morogoro na makubaliano yamefikiwa na kesi hiyo kutolewa nje ya Mahakama; na wamefikia settlement agreement ambayo wanaweza kuendelea na shughuli zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, lilihusu VAT returns, nami nitumie nafasi hii kuishukuru Wizara ya Fedha kwa dhati kabisa na kuwashukuru TRA, wameonesha commitment na wame-deploy team kwa kampuni zote za tobacco kuweza kupitia VAT returns zao za muda mrefu na mwezi huu wa Novemba mwishoni ndiyo yalikuwa makubalino juu ya kusaini makubaliano ya transfer pricing na VAT returns. Hatua zinaendelea vizuri na wawekezaji wameonesha positive results kwa kuonesha kwamba hatua za Serikali zinachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya tatu ilikuwa ni suala la kesi za FCC. Tumefanya vikao na Serikali imewaagiza FCC kukaa na wafanyabiashara hawa ili kuweza kutafuta njia sahihi ya kuwa na suluhu badala ya kuendelea kuwaadhibu kwa sababu inaathiri sekta ya kilimo na inaathiri Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama Serikali hatuna nia wala dhamira ya kuhakikisha kwamba kuna mwekezaji yeyote anaondoka, lakini akiondoka, ataondoka kwa mujibu wa sheria; na kwenye ubinafsishaji kulikuwa kuna mkataba na taratibu za kurudisha mali hizo ziendelee kubaki ndani ya nchi. Utaratibu upo katika mkataba waliobinafsishiwa infrastructure zote kuanzia kiwanda na magodauni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba mali zote za Watanzania zitaendelea kubaki kwa ajili ya maslahi ya Watanzania.
MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri; na kwa kweli nikiri kwamba huyu kijana ameanza vizuri na uendelee vizuri hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kulishughulikia suala hili la tumbaku kwa hasa huyu mwekezaji TLTC ambaye anaondoka; TLTC alikuwa anafanya biashara na vyama 97 hapa nchini. Katika hivyo 97, Chunya nina vyama sita au saba ambavyo vilikuwa vinafanya biashara naye na mpaka sasa hajatoa makisio. Kwa hiyo, kuna wasiwasi kwamba kwa msimu huu tunaoanza nao haviwezi kufanya biashara.

Je, Serikali itazibaje pengo hili ili vyama hivi 97 nchi nzima vifanye biashara mwaka huu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwatoe hofu wakulima wa Chunya, Tabora na maeneo mengine, waendelee kuandaa mbegu zao, kwa sababu tuna maongezi na kampuni ya British American Tobacco ambao tumefanya kikao mwezi huu wa Novemba tukiwa Wizara ya Kilimo na Wizara ya Fedha. Mchakato wa maombi hayo umeenda Wizara ya Fedha, unaendelea kuangaliwa. Vile vile wameonyesha nia ya kununua kilo milioni nane kutoka kwa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwatoe hofu wakulima wa maeneo ya Chunya kwamba waendelee kufuata utaratibu wa best practice ya kuzalisha tobacco, wasiwe na hofu. Ni dhamira ya Serikali kumwongeza player mwingine ndani ya soko la tobacco.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile TLTC hivi karibuni viongozi wao watakuja kuongea na Serikali; wameshaonesha nia ya kurudi sokoni. Kwa hiyo, tuendelee kuvuta subira na niwatoe hofu wakulima wa tumbaku kwamba suala la TLTC litafika mwisho, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba tunaondoa tatizo hili. (Makofi)
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri katika dhana nzima ya uchumi kukua ukioanisha na maisha ya wananchi, kinadharia kwa kweli alivyosema ni sahihi kabisa na napenda nipongeze kwa Serikali ya Awamu ya Tano ambayo imekuwa ikifanya kazi sasa kurekebisha na kurahisisha maisha ya wananchi yaweze kuwa na unafuu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza; uhalisia wa maisha sasa hivi kwa wananchi ni ghali zaidi na hali ya maisha ya wananchi bado ni ngumu. Je, Serikali inaweka mkakati gani pamoja na kuonesha kwamba hata mkulima wa pamba ambaye anauza pamba yake anakopwa halipwi na bado anategemea ahudumie baadhi ya gharama zake mwenyewe, je, ni lini Serikali sasa itaachana na mtindo huu kwa kutoa guarantee kwa wakulima wa mazao yote ili waweze kuwa wanapewa bei ambazo zinawakomboa katika shughuli zao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; sasa hivi bei ya vyakula inazidi kupanda na ukiangalia wananchi wengi wanaathirika na kupanda kwa bei ya vyakula. Gunia la mahindi sasa ni karibu Sh.100,000, je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza gharama hizi za maisha kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Chegeni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, dhana ya kupanda bei, kushuka bei ni relative. Ni Bunge hilihili mwaka jana wakati bei ya mahindi kwa mkulima ilikuwa Sh.150, ni Wabunge hawahawa walilalamika na kusema kwamba kwa nini tunafunga mipaka. Sisi kama Serikali kupunguza gharama za bei sokoni hatua tunazochukua; moja ni kupunguza gharama za uzalishaji, mbili kuruhusu soko ku-compete, competition ndiyo itakayopunguza bei ya mazao sokoni. Pale ambapo mkulima anapata hasara hakuna mtu anayekwenda kum- subsidize. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kama Serikali hatua ya kwanza hatutaingilia bei kushusha, nini tunafanya; tunayo National Food Reserve Agency na nitumie Bunge hili kuwaambia Waheshimiwa Wabunge na Wakuu wa Mikoa; pale ambapo wanaona kwamba kuna upungufu wa mazao ya chakula sokoni wawasiliane na National Food Reserve Agency ambayo ita-supply chakula katika maeneo hayo ili kupunguza presha, lakini hatutaingilia kupunguza bei ya mazao kwa sababu wakulima wa nchi hii kwa muda mrefu wamepata hasara kwa kuwafanyia control mazao yao. Huu ni msimamo wa Serikali na ieleweke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, njia ya pili, tunahamasisha Watanzania, ardhi ya Tanzania ni potential kwa kilimo, watu wafanye jitihada kuongeza uzalishaji. Supply ikiwa kubwa, demand ikiwa ndogo mazao yatashuka bei, lakini hatutafanya intervention yoyote kwenda kupunguza bei. Njia pekee tunayofanya kama Serikali ni kutumia National Food Reserve Agency kwa ajili ya ku-supply mazao ya chakula sokoni na kupitia NFRA bei itapungua, lakini kusema bei ya chakula iko juu ni relative; ni saa ngapi bei ya chakula iko chini, ni saa ngapi bei ya chakula iko juu. Kitu cha muhimu ni kufanya jitihada kama nchi kuongeza purchasing power ya watu wetu na wakulima wetu waweze kufaidika. (Makofi)

SPIKA: Lile la pamba?

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, tatizo la pamba lililojitokeza mwaka huu ni special case. Ni kama ilivyojitokeza kwenye korosho mwaka jana; Serikali ilifanya intervention. Intervention tulizozifanya mwaka jana, mwaka huu hatukuzitumia, tumeruhusu soko, minada inaendelea, wakulima wanapata pesa yao on time na competition iko wazi.

Mheshimiwa Spika, tatizo la pamba lilijitokeza katika msimu uliopita niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, halitajitokeza msimu ujao, tutaruhusu soko, hatutafanya kutangaza control ya price, Serikali itakachokifanya kwa wakulima wa pamba wasipate hasara ni ku-control gharama za input kuanzia viuatilifu, mbegu na mambo mengine, lakini siku ya mwisho sokoni tutaruhusu bei ili wafanyabiashara waende wakutane na wakulima sokoni waweze kununua bidhaa ile na mtu apate pesa yake kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, hii ilikuwa ni special case kwa sababu bei ya pamba duniani imeanguka na sababu ya kuanguka ni kwa sababu ya mtikisiko na mgogoro uliopo kati ya China na Marekani, matokeo yake pamba imekosa bei. Serikali ikaamua kutangaza bei ya Sh.1,200 na ili wafanyabiashara wasipate hasara tukaamua kufanya mazungumzo na financial institution kuwapa incentive ili waweze kwenda kununua kwa bei ya Sh.1,200.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa wakulima wa pamba mpaka kufikia siku ya Ijumaa wamelipwa bilioni 437, ambacho hakijalipwa ni bilioni 43 tu ndizo ambazo hazijalipwa na sisi tunafanya jitihada kuhakikisha by the end of this month wakulima wa pamba waweze kulipwa fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili ili wasipate shida kwa sababu msimu unaanza tarehe 15, nitumie nafasi hii kuwaambia wasambazaji wa mbegu wote wawasambazie wakulima bila kuwauzia halafu tuta-recover gharama ya mbegu msimu utakaokuja. Sasa hivi wakulima waende shambani kwa sababu malipo yalichelewa, lakini wapo ambao hawajalipwa, kwa hiyo wapewe mbegu.

Mheshimiwa Spika, namwelewa Mheshimiwa Dkt. Chegeni, moja ya wilaya ambazo zimeathirika sana ni Wilaya ya Mheshimiwa Dkt. Chegeni, lakini tatizo hili halitajiruudia msimu ujao. Nashukuru.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa bahati Mheshimiwa Naibu Waziri ameanza kwa kusema kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ni mwendelezo wa Serikali zilizopita.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, zao la kahawa linaelekea kupotea kwa kasi kubwa sana na sababu kubwa inalolifanya zao hili hili lipotee ni mabadiliko ya tabianchi. Je, Serikali ina mkakati gani wa kufanya utafiti upya ili kuleta mbegu ambazo zitaendana na hali ya hewa ambayo ipo sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri amesema kwamba mazao haya yalikuwa ni mkakati kwa ajili ya malighafi za viwanda. Sasa nataka aniambie, tulikuwa na kiwanda cha VOIL pale Mwanza, Kiwanda cha Magunia Morogoro, Kiwanda cha Magunia Moshi, tulikuwa na Kiwanda cha Nyuzi Tabora. Hivi viwanda havipo ilhali wananchi wanaendelea kuzalisha: Je, hizi malighafi wananchi wanazozalisha, zinakwenda katika viwanda vipi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, suala la mabadiliko ya tabianchi ni challenge ambayo inaikabili nchi yetu na dunia kwa ujumla. Wizara ya Kilimo kupita taasisi yake ya TARI sasa hivi tunafanya utafiti wa kuwa na mbegu sitakazokabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Hii imeonekana katika korosho ambapo tumepunguza muda wa mpaka zao la korosho kuja kuzalisha matokeo. Kwa hiyo, tunafanya hivyo hivyo katika mazao yote ya kimkakati na hata mazao ya chakula.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utafiti huu unaendelea pamoja na soil profiling ili kuweza kujua kwamba eneo hili ambalo tunalima kahawa je, bado litaweza kuhimili zao la kahawa au ama tuweze kuwashauri wananchi jambo lingine? Sasa hivi Wizara kupitia taasisi yake ya TARI inaendelea na utafiti katika vyuo mbalimbali lakini wakati huo huo tunafanya suala la soil profiling.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto ya tabianchi, zao la kahawa linakabiliana na changamoto nyingi ikiwepo mfumo wa uzalishaji na mfumo wa uuzaji kupitia ushirika, Wizara inapitia mfumo mzima wa kuanzia uzalishaji mpaka uuzaji wa mazao yote ili kuweza kuleta tija kwa mkulima.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la viwanda ni ukweli usiofichika kwamba Taifa letu limepitia nyakati mbalimbali na viwanda vyetu vingi vimepitwa na teknolojia. Sasa hivi Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda na Biashara tunafanya mapping na ku-develop new strategy ili ku-attract investors ili waje kuwekeza katika Sekta ya Viwanda ili waweze ku-take off mazao ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Nyuzi Tabora na viwanda alivyovitaja Mheshimiwa Waziri vikiwemo viwanda vya pamba, sasa hivi vingi vimepitwa na teknolojia. Tunaposema tunafufua, sisi kama Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda tumekubaliana mkakati wetu siyo suala la kufufua tu ni ku-attract uwekezaji mpya utakaoendana na teknolojia ya sasa ili mazao ya kilimo yaweze kupata tija na kuweze kupata masoko ya uhakika. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Zao la kahawa ni miongoni mwa mazao ya kimkakati, lakini zao hili bei yake imekuwa ikisuasua kila mwaka; na ukilinganisha uzalishaji wa zao hili kwa mkulima gharama zinakuwa kubwa:-

Nini mkakati wa Serikali ili kuweza kuongeza bei ya kahawa ili mkulima aweze kuendeleza zao hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, kwanza mkakati wa Serikali ni kutambua gharama halisi za uzalishaji za wakulima. Wizara ya Kilimo chini ya Naibu Katibu wa Mkuu Prof. Tumbo, sasa hivi tumeanza program ya kuanza kufanya evaluation ya mazao yote kujua mkulima anatumia shilingi ngapi.

Mheshimia Spika, kuhusu zao la kahawa, kama nilivyosema wakati namjibu Mheshimiwa Shangazi, ni kweli linakumbana na changamoto nyingi. Changamoto ya bei ya ni matokeo ya mfumo ambao umekuwepo muda mrefu ambao umemnyonya mkulima. Sasa hivi tunatumia Benki ya TADB ambayo imeanza kuzipa fedha taasisi za ushirika zilizopo katika Mkoa wa Kagera ili waanze kuchukua mazao ya wakulima kwa bei maalum na wakati huo huo tukitafuta masoko ya uhakika.

Mheshimiwa Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge watupe muda kama Wizara, mazao yote haya tutayabadilisha mfumo wake na kuruhusu sekta binafsi iwe competitive wakati huo huo tukipunguza gharama za uzalishaji kama Serikali ili mkulima awezi kupata faida.
MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya kwa ajili ya kuimarisha ushirika, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa huko nyuma tulikuwa na Mara Corp, tulikuwa na SHIRECU, tulikuwa na Nyanza, tulikuwa na KCU. Viongozi wake walikuwa na nguvu, weledi na uwezo, lakini vyama vile vya ushirika vilikuwa na mitaji kiasi kwamba vile vyama vya ushirika ndiyo vilivyonunua mazao ya wakulima na siyo kununua peke yake, hata kusindika na mfano ni Mkoa wa Mara, tulikuwa na Kiwanda cha Mwatex na Mwanza walikuwa na Mutex na Mwanza, lakini tulikuwa na Mgango Ginnery, tulikuwa na Ushashi Ginnery, tulikuwa na taasisi mbalimbali kwa ajili ya kusindika mazao ya wakulima. Sasa ushirika huu umeanza, viongozi wake hawana weledi, hawana mafunzo, lakini ushirika hawana mitaji na viwanda vile vya kusindika mazao vingi vimekufa.

MWENYEKITI: Uliza swali sasa.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujua Serikali ina mkakati gani kuhakikisha inapatia ushirika mitaji ili vyama hivi viweze kujiendesha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa tulianzisha Benki ya Kilimo kwa ajili ya kuwakomboa wananchi na hasa wanawake na kwa kuwa vipo vikundi vingi vya wanawake vilivyoanzishwa kwenye SACCOS kwa ajili ya kilimo, ningependa kujua Benki ya Kilimo itafika lini kwa ajili ya kuwakopesha wanawake vijijini katika ushirika wao wa kilimo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mfumo wa ushirika wa SHIRECU na vyama vingine vya ushirika wakati ambao anaongelea Mheshimiwa Mbunge, mfumo wa uchumi ambao nchi ilikuwa inaenda nao ulikuwa ni mfumo hodhi. Kwa hiyo mfumo ule wa ushirika wa wakati ule ulikuwa ni compatible na zama zile na wakati ule. Sasa hivi ni mfumo wa soko, hatuwezi kurudi katika mfumo uliokuwepo wakati wa nyuma. Lakini tunachokifanya sisi kama Serikali sasa hivi ni kupitia upya Sheria ya Ushirika ya mwaka 2002 wakati huohuo kupitia Sheria ya Ukaguzi ya Vyama vya Ushirika ya mwaka 1985 na kupitia mfumo mzima wa uendeshaji wa ushirika ili vyama vya ushirika viweze kuwa vya kibiashara na vijiendeshe kibiashara zaidi na kuwa competitive katika soko ambalo ni soko huria linaloruhusu watu binafsi kufanya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu suala la ushirika kupewa mitaji na Serikali; hili jambo haliwezekani. Kisera ya kiuchumi hatuwezi Serikali kuwapelekea vyama vya ushirika kupewa mitaji ya kujiendesha, lakini Serikali inachoweza kukifanya ni kuvifanya vyama vya ushirika kuwa strong na viweze kukopesheka na viweze kufanya biashara ili viwe vina sura ya kuendesha na kutengeneza faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Benki ya TADB; TADB ni development bank na wala siyo commercial bank kama benki zingine, haiwezi kufungua matawi nchi nzima, lakini pale ambapo ama chama cha ushirika au wananchi ambao wanaendesha miradi ya kilimo ya kimkakati wana business plan wanaweza kwenda ku-access mikopo katika Benki ya Maendeleo ya Kilimo ili tuweze kuendeleza infrastructure ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Waheshimiwa Wabunge wakaelewa, Tanzania Agricultural Development Bank ni development bank na siyo commercial bank, haiwezi kufanya kazi za commercial bank, inafanya kazi za kuwekeza kwa miradi ya muda mrefu kwenye sekta ya kilimo. Kwa hiyo hawawezi kwenda kufungua matawi katika wilaya na mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu akina mama; akina mama Tanzania Women Bank imeunganishwa na Postal Bank na facilities za akina mama kuweza kukopeshwa mikopo midogo midogo inapatikana kupitia Benki ya Posta kwa akaunti maalum ambayo imeanzishwa kama product kupitia benki ile.

Kwa hiyo, ninataka niwaombe Waheshimiwa Wabunge watusubiri wakati tunapitia Sheria ya Ushirika na kubadilisha mfumo wa uendeshaji wa ushirika ili uweze kuendana na mahitaji ya sasa na kuwajengea imani wananchi. Nashukuru. (Makofi)
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na kuwepo kwa wataalam watafiti wenye uwezo na weledi, taasisi nyingi za utafiti zinakabiliwa na changamoto kubwa za miundombinu mibovu lakini pia ukosefu wa rasilimali fedha pamoja na madawa kwa ajili ya kufanya utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haioni kwamba kushindwa kutenga asilimia moja ya bajeti kwenda kwenye utafiti inasababisha Serikali kushindwa kuhudumia taasisi hizi na hivyo kusababisha magonjwa kuendelea kutesa mimea na wananchi kuendelea kuathirika kwa kulima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Serikali ina mkakati wa kuweza kusambaza mbegu bora na miche bora ambazo zinahimili magonjwa wakati huo huo zinapandwa maeneo ambapo pambeni yake kuna mazao yaliyoathirika, kuna mimea iliyoathirika. Kwanini Serikali isije na mkakati sasa na program maalum ya kuondoa mimea iliyoathirika yote na kuwezesha wakulima kupata mbegu nzuri na miche bora ili kuhakikisha kwamba miche mipya inayopandwa haiathiriki na hivyo kusaidia wakulima kuinua uchumi wa familia na uchumi wa Taifa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sakaya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli ni maamuzi ya Kikanda na Kimataifa kwamba tutenge asilimia moja ya pato letu kwa ajili ya research na development lakini vilevile ni ukweli usiopingika kwamba bado mapato ya nchi na vipaumbele na matatizo yanayotukabili kama nchi ni mengi. Kwa hiyo, uwekezaji katika research pamoja na kuwa ni muhimu lakini hatujafikia lengo ambalo tumejiwekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tulichoamua kama Wizara ya Kilimo ni kwamba all resource zinazokuja kutoka kwa development partners na tarehe 19, Wizara ya Kilimo tutakuwa na kikao na development partners wanaowekeza katika sekta ya kilimo, fedha zote tutaelekeza katika research na seed multiplication program ili uwekezaji katika vyuo na taasisi za utafiti uweze kupata resource inayotosheleza. Tuondoe uwekezaji unaofanywa katika capacity building ambao unatolewa na taasisi za Kimataifa zinazowekeza katika sekta ya kilimo. Kwa hiyo, focus yetu katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka huu ni uwekezaji mkubwa wa fedha zote za donors na development partners zinazokuja katika sekta ya kilimo pamoja na uwekezaji wetu wa ndani kuwekezwa katika maeneo ya research na uzalishaji wa mbegu bora ambazo zitakabiliana na matatizo yanayotukabili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna changamoto pale ambapo ardhi imekumbwa na tatizo halafu tunapeleka mbegu mpya. Kama Wizara tumeamua kufanya mapping na tumeanza programu katika Mkoa wa Dodoma, Wilaya ya Kondoa ambao wameathiriwa na sumukuvu. Maeneo yote haya sasa hivi tunaanza utaratibu wa kwenda kwa wananchi katika kata zilizoathirika kuondoa mbegu walizohifadhi kwa ajili ya msimu ujao na kuanza utaratibu wa kuwapatia mbegu mpya na ku-treat ile ardhi ili tatizo hilo lisiweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utaratibu wa kufanya mapping na kuelewa wapi kumeathirika na nini unaendelea ndani ya Wizara. Tunaamini kwa mpango mpya wa miaka mitatu wa Wizara ya Kilimo wa kuwekeza katika research na development katika taasisi hizi, tutaondoka katika matatizo haya yanayotukabili sasa hivi kama nchi.
MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO: Mheshimiwa Spika, nimesikia maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ambayo kwa ujumla wake swali langu la msingi halijajibiwa. Swali langu la msingi naulizia utoshelevu wa mbegu za mahindi na maharage kwa sababu ni mbegu ambao ni chakula. Je, kama nchi tunajitosheleza mbegu za mahindi na maharage kwa asilimia ngapi? Ndiyo msingi wa swali langu. Hii habari ya mtama, ufuta na ngano haikuwa msingi wa swali.

Mheshimiwa Spika, swali la pili nina hakika kuna uhaba mkubwa sana wa uzalishaji wa mbegu. Ni lini Wizara ya Kilimo sasa itakuja na mkakati unaoeleweka wa namna ya kukabiliana na tatizo hili na hasa ukizingatia kwamba Jeshi la Magereza na JKT kuna nguvukazi kubwa ambayo wanaweza kushirikiana na Wizara wakaja na mkakati wa kuondoa tatizo la mbegu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, tunataka majibu siyo maelezo tafadhali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Spika, mahitaji (potential demand) ya nchi ni metric tons 120,000 kwa mwaka. Asilimia 70 ya mahitaji haya ni mbegu za mazao ya nafaka ikiwemo mahindi. Ni ukweli usiopingika kwamba kama nchi tunajitosheleza kwa asilimia 40 tu ya mahitaji yetu ya mbegu ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, huu ndiyo ukweli na ndiyo status kwamba kama nchi tuna uwezo wa kuzalisha asilimia 40 ya tani 120,000 za mbegu ya mazao yote ndani ya nchi, kwa hiyo tuna upungufu wa asilimia 60 katika suala la uzalishaji kama nchi. Sasa hivi Wizara inafanya programu na siku ya Jumapili ya wiki hii taasisi zote zinazohusika na suala la uzalishaji wa mbegu za umma na binafsi tunafanya kikao Morogoro kwa ajili ya kutengeneza master plan ya miaka mitatu ili tuondokane na tatizo la import za mbegu na gap iliyopo katika suala la mbegu katika nchi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kuhusisha Taasisi za Umma kama JKT, Magereza katika grand plan ya miaka mitatu ya Wizara ya kufanya seed production, research na seed multiplication na soil profiling, JKT na Jeshi la Magereza ni sehemu ya mkakati wetu. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko kwamba kama Wizara tunafahamu upungufu na kama Wizara tumeamua kimkakati uwekezaji wa development partners wote tutaupeleka kwenye seed production, research na seed multiplication kwa kutumia irrigation ili tuondokane na suala la uzalishaji wa mbegu wakati wa msimu wa mvua. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali, kuna shida kubwa sana kwa waletaji wa pembejeo kwenye majimbo yetu. Jimbo la Rungwe linalima sana mazao ya viazi, lakini kumekuwa na ucheleweshwaji wa pembejeo. Tunaomba kujua Serikali inafanya mbinu gani ya kuhakikisha wanaoagiza pembejeo wanaleta pembejeo kwa wakati kwa wakulima?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, wawekezaji na hasa hao wabia ambao mnawapa kazi hiyo ya kusambaza pembejeo wanaleta pembejeo nyingine hazina viwango na hivyo kusababisha kupata mazao hafifu kwa kuwa pembejeo iliyoletwa si sahihi kwa wakulima wetu. Je, ni hatua gani itachukuliwa kuhusiana na suala hili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza utaratibu wa kuagiza pambejeo tunatumia mfumo wa bulk procurement. Utaratibu huu tender hutangazwa ambapo waagizaji wote wa mbolea wanakuwa wamesajiliwa na wanashindanishwa na kupewa time limit ya uagizaji na ku-deliver katika kila mkoa.

Mheshimiwa Spika, mfano kwa mwaka huu mahitaji yetu ya mbolea kwa nchi nzima ni jumla ya tani 700,000 na ambazo zinatakiwa ziwe delivered kuanzia mwezi wa 11 na jambo hilo limeendelea na mpaka sasa hatujapata tukio lolote la ukosefu wa pambejeo katika mikoa yetu. Kwa hiyo, kama kuna case inahusu maeneo ya Rungwe, nitamuomba Mheshimiwa Mbunge anipe hiyo specific case li tuweze kuifuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la ubora, Wizara ya Kilimo kupitia mamlaka yetu iliyokuwa ikiitwa TPRI ama kwa sasa inajulikana kwa mujibu wa sheria tuliyopitisha katika Bunge lililopita TAFA, tunafanya ukaguzi katika maduka yote yanayouza pembejeo. Pale ambapo tutakutana na pembejeo fake tunachukua hatua za kuwapeleka Mahakamani. Mpaka sasa kuna zaidi ya kesi tano za wasambazaji ambao walikutwa wana pembejeo fake.

Mheshimiwa Spika, ili kulitatua tatizo hili sasa hivi kwa sababu biashara ya pembejeo inafanyika katika wilaya, Wizara ya Kilimo sasa hivi tuko katika hatua za mwisho za kuanzisha kitu tunaita Customer Service Centre ambapo mkulima popote alipo katika nchi hii ataweza kupiga simu bure pale ambapo aidha kakutana na pembejeo fake ama kapata tatizo lolote la kiuatilifu ama tatizo la ugonjwa katika eneo lake na sisi kuweza kumhudumia kwa wakati. Tunachukua hatua hii ili kupunguza tatizo la gap ya muda kati ya athari inapotokea mpaka pale huduma inapoenda kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachosisitiza unapoenda kununua pembejeo popote hakikisha umepata risiti ya muuzaji ya EFD ili tutakapokuta kuna tatizo tuweze kumchulia hatua. Hili la Rungwe, kama kuna special case, karibu.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru japo sijaridhishwa hata kidogo na majibu ya Serikali kwa sababu malalamiko ya wananchi kwenye vyama hivi ni makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize swali la kwanza la nyongeza; kwa kuwa kumekuwa na malalamiko makubwa ya ubadhirifu wa Vyama hivi vya Ushirika, Bodi hizi kuwa wababe, kutoshirikisha wananchi, lakini pia mashamba haya kukodishwa pasipo tija kwa wananchi. Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa wa kuunda Tume Maalum itakayoshirikisha vyombo vyote vya dola kwenda kufanya uhakiki wa mashamba haya yote 17?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa sasa tunaona Sheria ya Ushirika ya mwaka 2013 haitoi fursa kwa viongozi wa ngazi ya mkoa kushuka chini kuweza kuona kinachoendelea kwenye vyama hivi vya ushirika. Je, Serikali haioni ni wakati muafaka wa kufanya mabadiliko ya sheria, ili sasa viongozi wa ngazi ya mkoa waweze kushiriki na kuona nini kinaendelea kwenye vyama hivi vya ushirika?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Saashisha kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna changamoto za baadhi ya Viongozi wa Vyama vya Ushirika kuhusishwa na ubadhirifu na Serikali imekuwa ikichukua hatua mara kwa mara. Tumeona hatua ambazo zimechukuliwa na Serikali katika Vyama vya Ushirika vya Tumbaku, tumeona hatua ambazo Serikali imechukua katika Vyama vya Ushirika vya Pamba, tumeona hatua ambayo Serikali imechukua katika Vyama vya Ushirika vya Mkonge.Hatua hizi zote zimechukuliwa na Serikali kuhakikisha kwamba kwanza mali zilizoibiwa za vyama vya ushirika zinarudishwa kwa wanachama, lakini mbili kuwachukulia hatua viongozi wote waliohusika na kuwapeleka katika vyombo vya sheria.

Suala ambalo analisema la uwepo wa Tume, ipo Timu Maalum chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo inafanyakazi hii na imekuwa ikiendelea kufanyakazi hii katika maeneo yote yanayohusu vyama vya ushirika na kama kuna specific case inayohusu Wilaya ya Hai namkaribisha Mheshimiwa Mbunge aje atueleze Wizarani na tutashirikiana naye kuhakikisha kwamba ubadhirifu kama upo katika maeneo ya Hai ya Vyama vya Ushirika vya Wilaya ya Hai, au Mkoa wa Kilimanjaro tutaweza kuchukua hatua kama ambavyo tumechukua hatua katika masuala yanayohusu mali za KNCU.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mabadiliko ya sheria kwanza ni vizuri Waheshimiwa Wabunge tukaelewa dhana ya ushirika ni dhana ya hiyari. Ushirika siyo mali ya Serikali ni mali ya washirika, lakini Serikali inaingilia kwenye masuala ya ushirika kwasababu ya public interest kwasababu ile inakuwa ni mali ya umma ndiyo maana tunayo Tume ya Ushirika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la upungufu wa kisheria Wizara ya Kilimo sasa hivi inaipitia sheria na mwaka jana ilikuwa tuilete ndani ya Bunge ili kuweza kuihuisha iweze kuendana na mahitaji ya sasa, badala ya kuwa ushirika wa huduma uwe ushirika wa kibiashara kwa maslahi ya wanaushirika. Kwahiyo suala la kisheria tunaliangalia na ni suala genuine ambalo Mheshimiwa Mbunge amelisema na muda ukifika tutaileta sheria ndani ya Bunge ili iweze kwenda na wakati, lakini siyo kuifanya Serikali i-control ushirika bali tunatengeneza sheria kuufanya ushirika ujiendeshe wenyewe kwa maslahi ya washirika na kutengeneza governing bodies ambazo zitausimamia ushirika kwa maslahi ya wanaushirika.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali, kuna shida kubwa sana kwa waletaji wa pembejeo kwenye majimbo yetu. Jimbo la Rungwe linalima sana mazao ya viazi, lakini kumekuwa na ucheleweshwaji wa pembejeo. Tunaomba kujua Serikali inafanya mbinu gani ya kuhakikisha wanaoagiza pembejeo wanaleta pembejeo kwa wakati kwa wakulima?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, wawekezaji na hasa hao wabia ambao mnawapa kazi hiyo ya kusambaza pembejeo wanaleta pembejeo nyingine hazina viwango na hivyo kusababisha kupata mazao hafifu kwa kuwa pembejeo iliyoletwa si sahihi kwa wakulima wetu. Je, ni hatua gani itachukuliwa kuhusiana na suala hili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza utaratibu wa kuagiza pambejeo tunatumia mfumo wa bulk procurement. Utaratibu huu tender hutangazwa ambapo waagizaji wote wa mbolea wanakuwa wamesajiliwa na wanashindanishwa na kupewa time limit ya uagizaji na ku-deliver katika kila mkoa.

Mheshimiwa Spika, mfano kwa mwaka huu mahitaji yetu ya mbolea kwa nchi nzima ni jumla ya tani 700,000 na ambazo zinatakiwa ziwe delivered kuanzia mwezi wa 11 na jambo hilo limeendelea na mpaka sasa hatujapata tukio lolote la ukosefu wa pambejeo katika mikoa yetu. Kwa hiyo, kama kuna case inahusu maeneo ya Rungwe, nitamuomba Mheshimiwa Mbunge anipe hiyo specific case li tuweze kuifuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la ubora, Wizara ya Kilimo kupitia mamlaka yetu iliyokuwa ikiitwa TPRI ama kwa sasa inajulikana kwa mujibu wa sheria tuliyopitisha katika Bunge lililopita TAFA, tunafanya ukaguzi katika maduka yote yanayouza pembejeo. Pale ambapo tutakutana na pembejeo fake tunachukua hatua za kuwapeleka Mahakamani. Mpaka sasa kuna zaidi ya kesi tano za wasambazaji ambao walikutwa wana pembejeo fake.

Mheshimiwa Spika, ili kulitatua tatizo hili sasa hivi kwa sababu biashara ya pembejeo inafanyika katika wilaya, Wizara ya Kilimo sasa hivi tuko katika hatua za mwisho za kuanzisha kitu tunaita Customer Service Centre ambapo mkulima popote alipo katika nchi hii ataweza kupiga simu bure pale ambapo aidha kakutana na pembejeo fake ama kapata tatizo lolote la kiuatilifu ama tatizo la ugonjwa katika eneo lake na sisi kuweza kumhudumia kwa wakati. Tunachukua hatua hii ili kupunguza tatizo la gap ya muda kati ya athari inapotokea mpaka pale huduma inapoenda kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachosisitiza unapoenda kununua pembejeo popote hakikisha umepata risiti ya muuzaji ya EFD ili tutakapokuta kuna tatizo tuweze kumchulia hatua. Hili la Rungwe, kama kuna special case, karibu.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pia namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo kwa majibu yake mazuri na mkakati uliopo, lakini ukiangalia mkakati wa kuongeza uzalishaji kutoka tani elfu mbili, elfu tatu, elfu mbili mia nne kufika elfu tatu na mbia mbili hiyo bado ni asilimia 25 tu ya mahitaji ya dunia. Sasa kwa vile pareto inatumika kwa ajili ya kuua wadudu na hasa dawa za kuhifadhi mazao ambayo itapunguza cost, post harvest loss kwa nafaka zetu. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri agizo lake alilolitoa kuhusu taasisi yetu ya TARI ili waweze kuanza kufanya utafiti wa kuzalisha dawa kwa ajili ya kuondoa hii post harvest loss, lakini vilevile na dawa kwa ajili ya kuuwa wadudu wa mbu, ni lini hilo agizo lake litaanza kutekelezwa? Nafikiri ni muhimu sana tukichukulia ushindani ulioko kwenye nchi zetu za Afrika Mashariki wenzetu Kenya pamoja na Rwanda kama ulivyosema wewe mwenyewe wameshaanza huo uzalishaji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa vile Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumzia kuhusu zoning ambayo hairuhusu wanunuzi wengi kwenye eneo moja. Hiyo limekuwa ni changamoto kwa bei ya pareto kuwa ndogo sana kwa vile kunakuwa na monopoly ya hao wanunuzi. Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuna umuhimu wa kuruhusu wanunuzi wengi kwa kila eneo ili kuwepo na bei ya ushindani? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyingeza ya Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza agizo ambalo tumelitoa mwaka jana Serikali na sekta ya kilimo inatumia zaidi ya bilioni 150 kwa mwaka kwa ajili ya kununua input kwa maana ya gharama za viuatilifu na vitu vya namna hiyo. Ni kweli kwamba, pareto ni moja ya zao ambalo linaweza kutupunguzia gharama kwa kiwango kikubwa cha uagizaji wa viuatilifu. Wizara ya Kilimo mwaka jana tumewapa agizo watu wa TARI, hivi sasa tunavyoongea utafiti unaendelea ukihusisha sekta binafsi pamoja na kampuni ya PCT ambayo ndio kiwanda pekee kinacho-process kwenda kwenye crude level uzalishaji wa maua haya kwa ajili ya kupatikana dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuwahamasisha sekta binafsi ya Tanzania, ni commitment ya Serikali kuanzia taasisi zetu kama NFRA na CPB kuanza kutumia unga unaotokana na pareto kuzuwia wadudu waharibifu wanaoingia katika mazao kama mahindi na hii itatuongezea soko la ndani. Sisi kama Wizara tunatoa commitment kama kuna muwekezaji yeyote ambaye atazalisha kiuatilifu kinachotokana na pareto kwa ajili ya matumizi ya viuatilifu ndani ya nchi yetu tutampa contract ya kuhudumia zao na taasisi ambazo ziko chini ya Wizara ya kilimo. This is a commitment na tuko tayari kwa hiyo, tunahamisha sekta binafsi kuwekeza. Namfahamu Mheshimiwa Njeza ni mdau katika sekta hii na Mheshimiwa Rais alisema mabilionea karibu Wizara ya Kilimo tujadiliane juu ya hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu zoning. Hatuwezi kuondoa zoning kwenye suala la uwekezaji. Ni unfair mwekezaji kampatia huduma mkulima, kampa mbegu, kampa dawa, kampa ugani, halafu umruhusu mtu ambaye hajawekeza aende akanunue zao ambalo mwenzake kawekeza. Tutaendelea ku-protect zoning katika eneo hili, lakini tutafungua milango kwa yeyote anayetaka kuja kuwekeza kwenye sekta ya pareto, ili tuweze kuwapa thamani wakulima wetu na sisi ndani ya Wizara ya kilimo we are open for this. Nashukuru.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri na Serikali wamekiri kwamba takriban skimu 70 zina changamoto na kule Mng’aro hivi tunavyozungumza ni msimu wa mpunga lakini wanashindwa kwenda mashambani kwa kuwa skimu haiwezi ikaririsha maji kuelekea mashambani. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka sana kuhakikisha kwamba skimu hii ya Mng’aro inatiririsha maji kuelekea mashambani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kulikuwa na maelekezo ya Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Chama alipotembelea Mkoa wa Tanga kwa maana kwamba Wizara ya Kilimo itembelee ikaone skimu hizi. Kwa sababu kuamini ni kuona, je, Waziri yuko tayari sasa kutenga muda na nafasi kwenda kuziona skimu hizi ambazo ni muhimu sana kwa uzalishaji wa mpunga katika Mkoa wa Tanga?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya ngonyeza ya Mheshimiwa Rashid Shangazi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Wizara ya Kilimo kwenda Mlalo, hivi karibuni tulikuwa Mkoa wa Tanga na Mheshimwia Waziri Mkuu lakini bahati mbaya hatukuweza kufika Jimbo la Mlalo. Nakata nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa mimi mwenyewe niko tayari tukutane tupange ili tuweze kwenda pamoja katika maeneo ya Mlalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu suala la kukarabati skimu hizi tatu tulizozitaja, kwanza practically sasa hivi ni kipindi cha mvua kwa hiyo ukarabati itakuwa ni vigumu sana kuufanya. Nataka nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tumetenga fedha kupitia Tume ya Umwagiliaji kiasi cha shilingi milioni 30 kwa ajili ya kurekebisha skimu za Mlalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada tu ya msimu huu wa mvua kuisha Wizara ya Kilimo tutatumia mfumo ambao tumeutumia kama majaribio maeneo ya Ruaha na Jimbo la Mheshimiwa Lukuvi kwa kutumia force account kufanya marekebisho ya skimu hizi na wala hatutotumia wakandarasi, tutatumia vifaa vyetu wenyewe. Tutaenda kufanya hivyo immediately baada ya msimu wa mvua kuisha na tumetenga fedha kwa ajili ya skimu zake tatu.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Niweke kumbukumbu sahihi, siyo kweli kwamba wamemaliza kulipa vyama vyote; kuna AMCOS ya Rumulo ikiunganisha Vijiji vya Rugasha, Kibingo na Mrongo wamelipwa nusu ya malipo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza. Changamoto kubwa ambayo wakulima wanakutana nayo inayotokana na Vyama vya Ushirika ni kushindwa kuwapa fedha kwa wakati na sababu ni kwamba fedha inakopwa benki kwa asilimia 9. Serikali haioni ni wakati muafaka kwa benki za kilimo kupunguza riba kwenda mpaka asilimia 5, ili waweze kupata uwezo wa kulipa kiasi cha kutosha cha kahawa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, sasa tunafanya biashara huru kwa kilimo na biashara nyingine ikiwa ni sera ya Serikali. Nchi jirani kama Uganda wananunua kahawa kwa gharama au kwa bei nzuri. Ni kwa nini Serikali isitengeneze special arrangements kwa wakulima hata wa Kagera waweze kuuza kwa makampuni ya Uganda ambayo yanatoa bei iliyo nzuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nitashukuru akinipa facts za kwamba Chama cha Msingi alichokitaja hakijalipwa kwa sababu takwimu tulizonazo Wizarani na fedha zilizotolewa na TADB kwa ajili ya kulipa wakulima wa Mkoa wa Kagera tumelipa 100%. Kwa hiyo, kama kuna kiongozi yeyote wa Chama cha Msingi ama Chama Kikuu cha Ushirika hajafikisha fedha kwa wakulima hao, tutachukua hatua immediately kwa sababu ni uhujumu uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la bei ya Uganda; mwaka huu katika Ukanda huu wa Afrika Mashariki, ukitoa wakulima walioko katika nchi ya Rwanda ambao wana mkataba maalum na Starbucks ambapo sisi kama Serikali sasa hivi tumeanza maongezi nao kwa ajili ya kununua moja kwa moja kutoka kwa wakulima, wakulima wa Mkoa wa Kagera wameuza bei nzuri kuliko mkulima wa Uganda. Kama mna bei na facts kwamba kuna mnunuzi Uganda anatoa bei nzuri kuliko mnunuzi wa Tanzania, milango ya Wizara ya Kilimo iko wazi, karibuni mtuletee. Hata hivyo hatutaruhusu biashara isiyokuwa na contract; yenye clarity ya mambo mawili (bei na volume) kuliko kuwaambia wakulima kwamba tutanunua na mchezo wa butura umekuwa ukiendelea. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, hatutaruhusu mkulima kufuatwa shambani kununuliwa kahawa. Mheshimiwa Mbunge wewe ni mzoefu, Kagera kumekuwa na biashara inaitwa butura na biashara hii imekuwa ikisimamiwa na viongozi wenye mamlaka na nguvu ambao wamekuwa wakienda kununua kahawa kwa wakulima kwa Sh.500 na Sh.700 hatuwezi kuruhusu. Kama kuna tatizo la malipo katika Vyama vya Msingi, tushughulikie tatizo la ucheleweshaji wa malipo na wala siyo kuua mfumo tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la riba, mpaka sasa kupitia Tanzania Agricultural Bank ndiyo imekuwa benki ambayo imeshiriki katika kushusha riba kwa wakulima ambao wamekopa katika benki mbalimbali. Walianza na riba ya asilimia 11 Vyama vya Ushirika vya Kagera sasa hivi wamepewa kwa riba ya asilimia tisa.

Vilevile commercial banks zilikuwa zinawapa riba kwa asilimia 20 kwa guarantee ya kupitia TADB, mikopo hiyo wamekuwa wakipewa kati ya asilimia 13. Tumeanza mazungumzo na commercial bank ili riba katika sekta ya kilimo isizidi asilimia 10. Majadiliano haya yameanza na tunaamini tutafikia lengo hili kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wakulima wanapata mikopo yenye riba nafuu.
MHE. NDAISABA G. RUHOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Napenda kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na aliyoyasema yakitekelezeka basi Tanzania ndani ya kipindi cha miaka mitatu itakuwa inaongoza kwa uzalishaji wa kahawa ukiachia Ethiopia, Uganda, Cote d’lvoire pamoja na Kenya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niulize swali langu la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha miche milioni 20 inayotarajiwa kuzalishwa inawafikia wakulima wa Tanzania wakiwemo wananchi wa Wilaya ya Ngara kwenye Tarafa za Kanazi, Nyamiaga, Rulenge pamoja na Murusagamba?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Februari mwaka huu tutagawa katika Mkoa wa Kagera kuanzia tarehe 27 Februari, 2021, tutagawa jumla ya miche 1,000,000 kwa wakulima bure. Kwa hiyo hiyo ni sehemu na malengo tuliyojiwekea ni ugawaji wa jumla ya miche milioni 20.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na jibu la Mheshimiwa Waziri, je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa Vyama vya Ushirika ili waweze kuwalipa wakulima wa kokoa Wilaya ya Rungwe na Wilaya ya Kyela kwa wakati kwa maana mpaka sasa wanadai madeni yao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali inatambua kwamba kokoa ya Kyela na Rungwe ni kokoa bora baada ya kokoa ya Ghana.

Ni nini Serikali itafanya kuwawezesha wakulima hawa na kuwasimamia bei yao iongezeke maana hiyo uliyosema Mheshimiwa Waziri ya shilingi 5,000 bado ni ndogo, haitoshi kwa wakulima maana wao ndiyo wawekezaji wakubwa na wenye kazi kubwa katika ukulima wao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mwakagenda maswali yake mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kulipa wakulima kwa wakati, kwa utaratibu na mwongozo ambao Wizara ya Kilimo imeutoa, baada ya mnada, mkulima anatakiwa awe amepata fedha zake ndani ya saa 72. Huu ndiyo utaratibu ambao tumeuweka. Kwenye minada ya kokoa tumejenga utaratibu ambapo mkulima anapewa malipo ya awali kabla ya mnada na baada ya mnada hupewa fedha ambayo ni difference kati ya fedha ya awali na fedha ambayo mnada umefikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatua tunazochukua sasa hivi ni kuviwezesha Vyama vya Ushirika kupitia Tanzania Agricultural Development Bank kupata fedha kwa gharama nafuu ili waweze kuwa na uwezo wa kukusanya mazao kwa wakati na kuyapeleka mnadani na pale ambapo mnada unakuwa bei yake haivutii, wakulima waweze kusubiri mnada uweze kuwa na bei nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Vyama vya Ushirika vya Kokoa vilivyoko katika Mkoa wa Mbeya sasa hivi vina maongezi na Tanzania Agricultural Development Bank na sisi Wizara ni sehemu ya majadiliano hayo. Bado hatujaruhusu wachukue fedha kwa sababu riba ambayo iko mezani ni kubwa kwa kiwango cha asilimia 9. Kwa hiyo, tunaendelea na majadiliano na hili tutalirekebisha. Tumhakikishie tu kwamba tutaendelea kuboresha mfumo wa stakabadhi ghalani ili kupunguza gap kati ya mnada na fedha kumfikia mkulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ubora, ni kweli na ndiyo maana bei ya kokoa ya Tanzania imepanda kutoka Sh.3,000 mwaka 2017 na sasa imefika wastani wa Sh.5,000 kwa kilo. Bado sisi kama Wizara tunaamini kwamba kokoa yetu ni bora. Sasa hivi hatua tunazochukua, tumeanza utaratibu wa certification ili kuweza ku-meet International Standard ili na sisi tuwe na zile competitive advantage ambazo zinakubalika katika soko la dunia. Ni lazima bidhaa ile ithibitike kupitia kitu kinaitwa Global Gap Certification kwamba bidhaa hii ni organic.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hizi ndiyo hatua tunachukua na mwaka jana tulipitisha sheria ya TAFA hapa na sasa TAFA wanaanza kazi ya ku-certify mashamba ili yaweze kupata hiyo hadhi. Kwa hiyo, tunaomba mtupe muda tuko kwenye hatua nzuri tunaamini tunafika, Inshaallah.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya zao la kokoa iliyoko kule Mbeya ni sawasawa kabisa na changamoto ambayo zao la korosho kwenye Wilaya ya Liwale inakumbana nayo. Kwenye msimu uliopita 2018/2019 mikorosho yenyewe ilikuwa inakauka bila kujua sababu ni nini. Kwenye msimu huu uliopita kwa nje zinaonekana korosho ni nzima lakini ukizipasua kwa ndani zimeoza.

Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutuletea wataalam kwenye Wilaya ya Liwale waje kufanya tathmini au utafiti kujua ni nini changamoto za korosho Wilaya ya Liwale zinazosababisha wananchi wale wapate bei isiyoridhisha?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi tu siyo tuko tayari, timu ya Wizara ya Kilimo leo ina wiki mbili ikishirikiana na watu wa TAFA na Naliendele. Timu hii wako Mkoa wa Mtwara na wengine wako Ruvuma kuangalia athari zilizojitokeza katika msimu uliopita ili tuwe tuna majibu sahihi ni athari za kimazingira ama kuna attack kwenye mimea yetu.
MHE. ALLY A. J. MLAGHILA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa mfumo huu wa Stakabadhi Ghalani umewafanya wananchi na wakulima wa kokoa wasipate pesa papo kwa papo kama ambavyo Serikali leo imejibu; na kwa kuwa majibu ya Mheshimiwa Waziri ni tofauti kabisa na uhalisia ulioko kule field, je, anachukua hatua gani kwa watu ambao wametoa taarifa ambazo sio sahihi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa zao la kokoa linalimwa na watu kwenye nyumba/kaya zao na siyo mashamba makubwa na wanatumia muda mwingi kukusanya hizo kokoa kidogo kidogo na pesa zinazolipwa zinachukua muda mrefu na kwamba makampuni yanayonunua yanaanza kwanza kukubaliana wao kwa wao pamoja na makato makubwa, je, Serikali inachukua hatua gani kudhibiti haya matatizo yaliyopo kwa wakulima? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally, Mbunge wa Kyela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza anaposema taarifa tulizotoa sio sahihi; taarifa tulizotoa ni sahihi, wakulima wamelipwa kutokana na takwimu tulizonazo na uthibitisho tulionao. Kwa hiyo, kama ana kesi maalum ya mkulima ama wakulima ambao hawajalipwa atuletee hiyo kesi na tutaishughulikia kwa wakati na inavyostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba kupitia Bunge lako Wabunge wanapoinuka na kusema kwamba, kuna mkulima X hajalipwa na sisi Wizara tunapoomba kwamba, tuleteeni uthibitisho, tunaomba mtuletee uthibitisho, mjadala huu usiishie humu ndani. Mtuletee uthibitisho, ili tuweze ku- resolve tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, taarifa tulizotoa ni sahihi. Hoja iliyoko ya kwamba, mkulima anapovuna, anapokausha, anapopeleka kwenye chama cha msingi mpaka inapoenda kwenye chama kikuu ni vizuri tukaelewa kwamba, cocoa inakusanywa kidogokidogo; mkulima atavuna kilo moja, baada ya siku chache atavuna kilo kadhaa, baada ya siku chache atavuna kilo kadhaa atapeleka kwenye chama cha msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna hoja kwamba, tujadiliane kupunguza muda wa kutoka kwenye chama cha msingi kwenda kwenye mnada, lakini hatuwezi kurudisha mfumo ambao ni maarufu kama njemke ambao wakulima walikuwa wanafuatwa majumbani na wanakusanyiwa cocoa yao na wanapewa bei ndogo na walanguzi hao ndio wanapeleka kwenye mnada, hatutaruhusu huo mfumo. Kama kuna changamoto kwenye mfumo wa malipo, tuujadili huo mfumo wa malipo na kama Waheshimiwa wana maoni watuletee, lakini Wizara sasa hivi tunatengeneza utaratibu wa kuondoa mfumo wa kuhifadhi mazao ya cocoa kwenye maghala binafsi na yatatumika maghala ya Serikali. Tutaanza pia kuuzia katika AMCOS, badala ya kuleta kwenye chama kikuu cha ushirika, ili tuweze kupunguza time kati ya mnada na malipo ya mkulima. (Makofi)
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Waziri, lakini naomba sasa niseme kwamba sasa ni miaka karibu saba tangu mmelitwaa hili eneo.

Je, haiwezekani kwamba mtachukua tena miaka saba kwa ajili ya kulirekebisha na kuweka mpango huo? Niombe basi kama nilivyosema kwamba wananchi wa Temeke tunatamani kujenga shule za sekondari na msingi kwa sababu tunazaliana sana na maeneo mijini sasa hivi hakuna. Niseme tu kwamba tuombe sasa Wizara yako itupe eneo hili ili sisi katika miaka hii ambayo tumeambiwa tujenge shule za sekondari pamoja na msingi basi tuyapate kwa sababu naona mtakwenda tena miaka saba ijayo katika kutengeneza hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; je, Serikali yetu sasa ina mpango gani wa kumalizia fidia kwa wananchi wa maeneo ya jirani karibu na pale ambapo mmetwaa lile eneo lakini yapo maeneo Shimo la Udongo ambapo mlitakiwa kuyatwaa lakini bado hamjalipa fidia. Naomba maswali yangu haya mawili tuweze kujibiwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nomba kujibu maswali mawili ya ziada ya Mheshimiwa Dorothy kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie hatutachukua miaka saba tena. La pili ni kwamba eneo lile ni karibu kabisa na Bandari ya Dar es Salaam na sisi kama Taifa tumekuwa mara nyingi tukijadiliana namna gani kuifanya bandari yetu kuwa effective na efficient na ili iweze kuhudumia waagizaji na wasafirishaji wa bidhaa. Itakuwa ni makosa ya kimkakati tukiligeuza eneo ambalo halizidi mita 500 au 1,000 kuligeuza kuwa eneo la shule. Nataka tu nimshauri yeye na Halmashauri ya Manispaa ya Temeke na Meya wake wa zamani yumo ndani ya Bunge hili ujenzi wa sekondari sio lazima tujenge kwenda…, tuna uwezo wa kujenga maghorofa kwa hiyo nawashauri Manispaa ya Temeke mjenge shule kwa mfumo wa maghorofa na ninyi mna mapato mengi kuliko Manispaa nyingi katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kuhusu fidia katika eneo lile tumebaki nadhani kaya kama mbili au tatu ambazo hazijamaliziwa fidia katika eneo la Kurasini na wale wananchi hawakuwa tayari, lakini wako katika hatua za mwisho kumalizana nao na watalipwa haki yao. Mpango wa Serikali katika lile eneo, eneo la ukubwa wa ekari 20 tunajenga The First Agricultural One Stop Centre ili mazo yetu ya kilimo hasa ya mbogamboga na matunda yaweze kusafiri kupitia Bandari ya Dar es Salaam badala ya sasa yanavyotumika kupitia bandari za nchi zinazotuzunguka.

Kwa hiyo, tunawaombeni sana watu wa Temeke mtuunge mkono kufikia azma hii ili eneo lile liweze kutusaidia kutatua changamoto ya usafirishaji wa mazao na kugeuza kuwa ni export hub eneo lile. Nashukuru.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; pamoja na majibu ya Serikali naomba kumuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, zao kuu la biashara katika Mkoa wa Tabora ni tumbaku je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mazungumzo na kampuni kubwa za kununua tumbaku ili kuweza kuongeza kilo zaidi wakulima wengi waweze kupata manufaa na kilimo hiki?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia wakulima wa Mkoa wa Tabora ili waweze kulima kilimo cha kisasa na waweze kupata zao bora la tumbaku ambalo linaweza kununuliwa katika soko la dunia? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hawa Mwaifunga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali imekuwa ikichukua jitihada za kuongea na kampuni mbalimbali za ndani na nje na ni vizuri Waheshimiwa Wabunge wakaelewa. Ni hatari sana kama nchi kuruhusu sekta kama ya tumbaku kuwa dominated na kampuni za nje peke yake. Hatua ya kwanza tuliyoichukua kama Serikali kwa mara ya kwanza tumeruhusu ushiriki wa kampuni za Kitanzania katika kununua tumbaku na tunazisaidia kupitia Balozi zetu za nje kuya- connect moja kwa moja na masoko ya Kimataifa. Sasa tuna kampuni nane ambazo zimeingia katika msimu uliopita na wamenunua tumbaku ya zaidi ya bilioni 12 kutoka kwa wakulima na wamekuwa na baadhi ya changamoto ambazo Serikali imekuwa ikiwasaidia. Lakini jitihada za kuongea na kampuni kubwa duniani, tuna maongezi na kampuni ya British American Tobacco, ambayo tunaendelea nayo maongezi. Tunajadiliana nao mfumo wa wao kuingia sokoni. Wao ombi walilolileta Serikalini ni kutaka kununua kupitia kampuni zilizoko hapa hapa za wenzao za nje na sisi hilo tumewazuia kwa sababu ita-restrict competition. Tunawataka waende moja kwa moja sokoni kushindana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ubora nataka tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kati ya wakulima wanaofuata best practice za kilimo katika nchi hii ni wakulima wa tumbaku na wakulima wa tumbaku wa Mkoa wa Tabora na mikoa mingine hasa Mbeya maeneo ya Chunya wanajitahidi sana kufuata utaratibu mzuri na hatua hii imesababisha hadi kupunguza madaraja ya mazao mabovu. Tumefuta madaraja kumi kwa sababu ya wakulima kufuata best practice. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba ubora wa tumbaku ya Tanzania hauna mashaka katika soko la dunia.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Changamoto ya soko la tumbaku inafanana kabisa na changamoto kubwa inayowapata wananchi wa Wilaya ya Chemba kwa soko la mbaazi pamoja na ufuta.

Je, ni lini Serikali itahakikisha wakulima wa Wilaya ya Chemba na maeneo yote Tanzania wanapata soko la uhakika kwa mazao ya mbaazi pamoja na ufuta? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunti kama ifuatavyo kwa niaba ya Waziri wa Kilimo:-

Kwanza nikiri katika kipindi cha mwaka mmoja, miwili iliyopita soko la mbaazi limekumbwa na changamoto. Sio sisi tu Tanzania peke yake bali nchi nyingi zinazozalisha mbaazi duniani na hii ilitokana na restriction iliyowekwa na nchi ya India. Lakini hatua iliyochukuliwa na Serikali, ni kufanya mazungumzo na hivi karibuni katika msimu ujao wa mbaazi restriction iliyokuwa imewekwa na India itakuwa imeondoka na tutakuwa na uhakika wa kuuza mbaazi katika nchi ya India. Mazungumzo yanaendelea na majadiliano yanaendelea. Nitamkaribisha Mheshimiwa Mbunge na baadhi ya Wabunge mwezi ujao tutakapokuwa na kikao cha wadau wa mbaazi, ufuta, choroko na dengu hapa Dodoma, Mwenyezi Mungu akijaalia kujadili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la ufuta, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali. Biashara ya mazao ni biashara ambayo kidogo ni complex, mkulima anapozalisha anapokuwa hana taarifa ya soko ndiyo maana Serikali sasa hivi tumeanza kutumia mfumo wa TMX kwa ajili ya price discovery na hii itatusaidia sana kuweza kupata the real value ya mazao ya kilimo na sasa hivi commodity market exchange yetu imeanza majadiliano na commodity market exchange za dunia. Kuna maongezi yanaendelea kati ya commodity market exchange ya Tanzania na commodity market exchange ya India na vile vile tumeanza maongezi na nchi ya China ili tuweze kufungua masoko haya na hatua zinaendelea kuchukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka ujao wa fedha Tanzania tutafungua the first display ya mazao yetu ya kilimo. Wizara ya Kilimo. tutaleta bajeti hapa ili Bunge lituidhinishie kufungua display ya mazao ya kilimo katika nchi ya China ili wafanyabiashara wetu wawe na eneo ambalo wana display mazao yao na kutafuta masoko moja kwa moja. Hii ni hatua ambayo tunachukua. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Tatizo kubwa la masoko ya tumbaku linafanana kabisa na tatizo la soko la korosho, lakini mimi nimegundua tatizo hili linasababishwa zaidi na kuwepo kwa mdudu mmoja anaitwa Vyama vya Ushirika. Vyama vya Ushirika vimekuwa vikiyumbisha sana masoko kwa wakulima wetu.

Je, Serikali iko tayari kuleta sheria ya Vyama vya Ushirika ili kuvifanyia marekebisho kuondoa matatizo yaliyoko kwenye vyama hivi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iko tayari kuleta sheria na tunafanyia mapitio sheria ya ushirika, lakini sio sahihi kufikiri kwamba mfumo wa ushirika ndiyo una haribu mfumo wa kuuza mazao, bali kuna washirika wanaoharibu vitu vya namna hiyo na Serikali imekuwa ikiwachukulia hatua. Lakini suala la sheria tuko kwenye mchakato na tutaileta Bungeni kuifanyia marekebisho. (Makofi)
MHE. JOSOPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Pamoja majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wetu wakiwemo wanawake na vijana wanatumia nguvu nyingi, wanatumia muda mwingi, lakini pia wanatumia pembejeo ambazo wanakuwa wamezikopa kwenye vikundi mbalimbali. Wanakopa pesa, wananunua mbolea na dawa; na wanapokuwa wamelima na wamevuna wanakosa soko hatimaye wanashindwa kulipa madeni pale walipo kopa pesa.

Je, Serikali ina mpango gani na inachukua hatua gani kuwa inauza mazao nje ya nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Genzabuke, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ni mmoja tu kati ya wanunuzi na sisi kama Wizara tumekuwa tukichukua hatua mbalimbali kwa ajili ya kusaidia Serikali yenyewe ama taasisi, ama wafanyabiashara wa Kitanzania kuuza mazao yetu nje ya nchi. Miongoni mwa hatua kama taasisi za Serikali, mfano Bodi yetu ya Mazao Mchanganyiko sasa hivi inaanza utaratibu wa kufungua mawakala katika nchi za Kongo, DRC na vilevile katika nchi ya Kenya kwa ajili ya kuuza mazao yetu moja kwa moja kupitia mawakala wa upande huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hatua nyingine ambayo tunachukua kama Serikali, ili kuhakikisha wakulima wanapata soko la uhakika ni kuzijengea uwezo taasisi zetu kwa maana ya NFRA na CPB na ndio maana nimesema katika jibu langu la msingi kwamba, sasahivi tuna mazungumzo na wenzetu wa hazina, ili kuruhusu taasisi zetu hizi mbili ziweze kuchukua fedha katika taasisi za benki na zinunue kama taasisi za kibiashara waweze kuuza mazao mbalimbali, lakini vilevile tunatumia balozi zetu kuwasaidia wafanyabisahara wa kitanzania kuuza mzao yetu yaliyochakatwa nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kupitia Bunge hili nataka niwaombe wachakataji wa mazao hasa ya mahindi, hakikisheni mashine zenu mmezifungia kitu kinaitwa fortification ili unga wetu uwe unga fortified na uweze ku- meet international standards. Hili ni jambo ambalo linatukwaza katika kuuza mazao nah ii ni peoject ambayo inatakiwa sekta binafsi waweze kuifanya. Kwa hiyo, Serikali inachukua hatua hizo. (Makofi)
MHE. DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa suala la masoko nje ya nchi limeendelea kuwa changamoto hususan baadhi ya bidhaa zetu, kwa mfano parachichi na hivi karibuni tumeona parachichi letu la Tanzania limefika nchi fulani na ikaharibiwa nje ya nchi.

Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na masoko haya ya nje ya nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pindi Chana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jitihada zinazofanywa na wenzetu hasa katika nchi zinazotuzunguka hasa nchi kama za SADC ku-sabotage wafanyabiashara wa Kitanzania kuuza mazao katika nchi zao wakati sisi kama nchi tunaruhusu kwa mujibu wa sheria na mikataba tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukio alilolitaja Mheshimiwa Mbunge ni tukio ambalo limetokea katika nchi moja iliyoko Kusini mwa Afrika. Tumeanza mazungumzo na wenzetu wa Foreign Affairs na mimi nataka niwahakikishie Wabunge, Tanzania imeshiriki katika ukombozi wa nchi nyingi katika Afrika, hatutaruhusu wafanyabiashara wetu kudhalilishwa kwa njia yoyote ile. Tutachukua hatua dhidi ya nchi hii na sisi tutazuia bidhaa zao pale ambapo itabidi kufanya namna hiyo. (Makofi)
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona. Naomba niulize swali la nyongeza kwa Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba uwepo wa taasisi kama NRFA na Bodi ya Mazao Machanganyiko ni pamoja na ku-act kama price stabilizer.

Je, ni hatua gani ambayo Serikali imechukua ili chombo hiki kiweze kutoa pesa na uwezo mkubwa ili kinunue mazao kwa wananchi tukijua kabisa kwamba majadiliano ya kupata guarantee Serikalini imechukua muda mrefu sana?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Kandege, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Wizara, tumeendelea majadiliano na hazina, lakini vilevile katika kipindi cha hivi karibuni taasisi yetu ya CPB imeweza kupata fedha kutoka katika mifuko ya hifadhi ya jamii zaidi ya bilioni saba na fedha hizo wameshaanza kurudisha kwa hiyo, wamekuwa credible na wameonesha proper business plan. Bado tunaendelea na maongezi na wenzetu wa Hazina na tutapata solution.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna maongezi na Benki ya CRDB na NMB katika ku-finance miradi ya CPB ya kununua mazao kwa kutumia collateral management system badala ya kusubiri kibali kutoka Hazina. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mazungumzo yetu yako katika hatua nzuri na tutafikia kule ambako siku zote yeye toka akiwa Kamati ya Bajeti akisukuma tutafika huko Mwenyezi Mungu akijalia hivi karibuni, Inshallah. (Makofi)
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na niipongeze Serikali kwa hatua ambazo imezichukua juu ya zao hili la michikichi, lakini vile vile nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameonesha jitihada za kipekee sana katika kusaidia zao hili la mchikichi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upungufu wa mafuta katika nchi yetu, niipongeze Serikali tu kwamba ni kweli imewekeza jitihada kwenye kuzalisha mbegu lakini napenda kujua Serikali imejiandaaje katika kuokoa mafuta yanayopotea kwenye Mkoa wetu Kigoma katika kuwekeza kwenye teknolojia? Kwa sababu kuna mafuta mengi sana yanapotea, hata hii miche iliyopo inapoteza mafuta mengi sana kabla ya kuwekeza kwenye miche mipya hii ambayo ameisema Naibu Waziri. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Makanika, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi Serikali tumeanza maongezi na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, TIRDO na SIDO kwa ajili ya kuja na teknolojia rahisi. Kwa sababu tume-invest katika miche baada ya miaka mitatu itaanza kutoa matokeo. Sasa itakapotoa matokeo tunakuja na mfumo wa ku-develop teknolojia ndogondogo ambazo katika household level, wananchi wataanza kukamua mafuta na kuyafanya kuwa crude ili yaweze kuzalishwa na kupunguza upotevu unaoongelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge amerudia jambo hili mara ya pili, katika Kamati vilevile ali- raise concern hii, nataka nimhakikishie kwamba tunajadiliana na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara ili kuja na teknolojia ya kupunguza hasara na upotevu.

Vilevile kuja na teknolojia rahisi ya ku-process mafuta katika primary level, katika level ya crude, pale ambapo miche hii itakuwa ime-mature na kuwafanya wakulima badala ya kuuza matunda wauze mafuta crude kwa processor wa secondary level.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na ninashukuru majibu ya Naibu Waziri ambao ndiyo uhalisia wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali lilikuwa ni kuwakomboa au kuwasaidia wakulima, na kwenye majibu yako, majibu ya Wizara, unasema kwamba Sekta binafsi zipo ambazo zinatoza riba kubwa. Ningependa kufahamu Wizara imefanya utafiti kiasi gani kujua ni kwanini Sekta Binafsi zinatoa riba kubwa kwenye matrekta? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa kuwa mfuko wa pembejeo uko ndani ya Serikali pamoja na Benki ya Kilimo ni kwanini sasa Serikali isiweke ruzuku kwenye hizo Sekta Binafsi kama ilivyofanya kwenye taulo za kike ili wananchi waendelee kupata neema kwenye hizo trekta? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aida kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kwanini Sekta Binafsi inatoa riba kubwa. Kkama Serikali na kwa muda mrefu tumekuwa na tatizo la model of financing kwenye Sekta ya Kilimo na ukiangalia financing model na mifumo mingi ya kutoa mikopo inakuwa ni mifumo inayofanana kuanzia grocery, kilimo na sekta zingine za uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kama Wizara hatua tuliyochukua, tumewasiliana na wenzetu wa Wizara ya Fedha, tumewsiliana na Benki Kuu ili kutengeneza mfumo sahihi unaoendana na Sekta ya Kilimo; na sasa tumeanza majaribio katika Sekta ndogo ya pamba. Kwa mara ya kwanza Sekta Ndogo yap amba tumeipatia mkopo kwa riba ya asilimia mbili. Tumetengeza a vehicle kupitia ushirika, na mwaka huu tumegawa dawa na pembejeo na mbegu bure kwa wakulima kwa gharama ya asilimia mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mfumo huo huo tunaufanyia majaribio safari hii kwenye sekta ya korosho. Kwamba wakulima watapata pembejeo zote za kilimo bure na tutarudisha gharama katika mjengeko wa bei lakini gharama ya financing hii itakuwa asilimia mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo ameunda timu ya wataalam ikiwahusisha wataalam kutoka Benki Binafsi na Benki Kuu ambayo tutapeleka ushauri Serikalini kupitia Benki Kuu ili tuwe na regulation za namna gani tutapata financing katika Sekta ya Kilimo ili itazamwe tofauti na sekta zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la ruzuku kuwa Sekta Binafsi, hili bado tunaliangalia kwa sababu tunaangalia insurance model. Kwa suala la kutoa ruzuku historia inaonesha ruzuku imetumika vibaya hata huko nyuma kwenye pembejeo, kwa hiyo hatuwezi sasahivi kutoa commitment kwamba tutatoa ruzuku katika taasisi binafsi ambazo zinakopesha. Lakini tumeanza kutumia Benki yetu ya Kilimo kwa mara ya kwanza sasahivi imetoa mikopo kwa asilimia 10, na sasahivi tunajadiliana nayo angalau mikopo ya vitendea kazi iweze kwenda kati ya asilimia tano na isizidi asilimia 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Waheshimiwa Wabunge, la muhimu zaidi mkulima anahitaji shamba lake lilimwe na trekta, lipandwe na planter, lipate boom sprayer. Si lazima mkulima wah eka moja a-own trekta. Tunachokifanya kama Serikali ni kuhamasisha Sekta Binafsi, na sasa tumepeleka pendekezo kwenye technical team ya kodi ili VAT inayochajiwa kwenye huduma za kilimo iweze kuondoka kupunguza gharama za wakulima kwa ajili ya kuwalimia. Kwa hiyo ni mchakato tunaomba Waheshimiwa Wabunge mtupe muda tunalifanyia kazi. (Makofi)
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Imekuwa ni changamoto kubwa sana kwenye masuala ya pembejeo hasa muda. Mara nyingi sana kwamfano jimboni kwangu kumekuwa na changamoto ya kuchelewa pembejeo kila muhula na hili jambo linajirudia mara kwa mara. Je, Serikali inaona jinsi gani ya kuweza kulitatua tatizo hili kwa haraka hasa hususan katiak msimu huu wa mwaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Mchungahela kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uchelewaji wa upatikanaji wa pembejeo una mahusiano ya moja kwa moja na upatikanaji wa fedha. Kw ahiyo tumebadili mifumo, sasa hivi tunatumia bulk procurement system ili tuweze kupata pembejeo kwa wakati na kwa bei nafuu. Tunaamini kwamba kuanzia msimu unaokuja kwa maeneo ya Lindi, Mtwara wanaolima korosho mtaona mabadiliko ya upatikanaji wa pembejeo.
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mojawapo ya mazao yanayoagizwa kwa kiasi kikubwa sana Uchina ni soy beans (maharage ya soya); na kwa mwaka Uchina wanatumia zaidi ya dola bilioni 40 na kuna nchi 12 tu ambazo zinaruhusiwa kupeleka maharage hayo kule Uchina. Tanzania ni nchi ya hivi karibuni ya 12 imeingia katika nchi hizo 12 na ndio ambayo iko karibu zaidi na Uchina ukilinganisha na zile nchi nyingine 11. Uzalishaji wetu ni mdogo sana na tumeshaingia mkataba wa kupeleka tani laki nne. Uzalishaji wetu kwa mwaka unaonekana kuwa kwenye tani 14,000 hivi.

Je, Serikali imejipanga vipi kutumia soko hili kubwa litakaloleta tija kwa wakulima hapa Tanzania? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Polepole kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba, hivi karibuni tumeingia makubaliano na Serikali ya China kwa ajili
ya kuwauzia soya. Nataka nitumie Bunge hili kuwataarifu Watanzania kwamba, consignment ya kwanza ya kupeleka soya tani 140 imesafirishwa mwezi Machi. Hatua tunazochukua za kwanza sasa hivi Taasisi yetu ya TARI na ASA tumewapa jukumu la kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa mbegu, hilo ni jambo la kwanza. Bajeti itakapokuja mwaka huu, mtaona tumetenga fedha kwa ajili ya kuyawezesha mashamba yote 13 ya ASA na kuyawekea mifumo ya umwagiliaji ili yaweze kuzalisha mbegu za kutosha za mazao mbalimbali na soya ikiwa mojawapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hatua ya awali, hatua ambayo tumechukua ili kuli-maintain soko hili, tumeamua kuondoa mifumo ya ukiritimba ya kuwasajili wafanyabiashara kwa ajili ya export. Kwa kuwa soko lipo na wafanyabiashara wapo, wakulima wenyewe wataongeza uzalishaji watakapopata mbegu za uhakika ambazo Wizara tunaanza kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tumefungua mlango wa re-export; tumewaruhusu wafanyabishara wa Tanzania, kwa kuwa, zao la soya pamoja na sisi kuwa tunazalisha, lakini linapatikana katika baadhi ya nchi zinazotuzunguka. Kwa hiyo, tumewaruhusu kwa mwaka huu wa kwanza, wakati tunajenga uwezo wa upatikanaji wa mbegu ya kutosha, waweze ku-import na waweze ku-re-export kwa sababu, bila ya hivyo tunaweza kulipoteza soko hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejipanga pia kuanzia mwakani mbegu zitakuwa za kutosha na tutawahamasisha wakulima waingie mikataba moja kwa moja na makampuni yote yanayosajiliwa, bure bila gharama yoyote, kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara na Wizara ya Kilimo. (Makofi)
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nilikuwa nina swali dogo moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tathmini inaonesha zaidi ya tani 200 za mazao aina ya alizeti zimeteketezwa na ndege hawa. Je, Mheshimiwa Waziri na Serikali wako tayari kupeleka mitego hii haraka kwenye Kata za Mwalu, katika Vijiji vya Mwalu, Minyuve, Mayaha, Ifyamahumbi, Kipunda, Maswea, Igombwe, Ihanja, Mahonda, Mtunduru, Songandogo pamoja na Gerumani ili kuweza kuwasaidia wakulima wetu kwa sababu, kwa kweli jambo hili liko very serious kwa wakulima wa alizeti katika Jimbo la Singida Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kingu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri Mheshimiwa Kingu amekuwa akifuatilia jambo hili kwa muda mrefu kwa ajili ya wananchi wake na yeye ndio aliyesababisha Wizara ya Kilimo mwaka jana mwezi Mei tukapeleka wataalamu kwa ajili ya kufanya tathmini na kuweza kutambua katika central corridor maeneo yenye maotea ya mazalia ya ndege hawa. Nataka tu nimwambie na nimpe commitment na kuwapa commitment wananchi wake na wananchi wa mkoa wa Singida kwamba Wizara kuanzia mwezi Mei itapeleka wataalamu na vitendea kazi kwa ajili ya kuanza kushughulika na wadudu hawa, ahsante.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lililoko Singida Magharibi ni sawa na lililoko katika Jimbo la Nkenge, Wilaya ya Misenyi na hasa wananchi wa Misenyi chakula kikubwa ni ndizi na baada ya kukumbwa na ugonjwa wa mnyauko ambao haujapata majibu majibu mpaka leo, wananchi wamejielekeza katika kulima mazao mengine mbadala. Mazao hayo yameendelea kushambuliwa na wanyama aina ya ngedere na hivyo kufanya wananchi hao kuhangaika sana kupata chakula.

Je, Serikali ina utaratibu gani kuweza kudhibiti wanyama hao waharibifu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kyombo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, labda tu niseme kitu kimoja na nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya maswali hapa tuweze kukutana na sisi kama Wizara tuko committed kupeleka wataalamu ili tuweze kupata solution ya wanyama hawa.
MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, changamoto katika Jimbo la Singida Magharibi inafanana na changamoto inayowakumba wananchi wangu wa Tihanga, Makutupora, Mchemwa, Nzansa na Gawale; na kwa kuwa kumekuwa na changamoto upatikanaji wa ndege ya kunyunyiza kwa wakati.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza ndege ya kunyunyiza kwa ajili ya udhibiti wa ndege na nzige, ili kuweza kuyafikia maeneo mengi kwa wingi na kwa muda mfupi zaidi kuliko ilivyo hivi sasa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anthony Mavunde, Mbunge wa Dodoma Jiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba sasa hivi kumekuwa na athari kubwa ambayo inatokana na ndege waharibifu, lakini vilevile wadudu na kama tulivyokuwa safari hii tumekuwa tukipambana mpaka sasa hivi na nzige na Wizara na Serikali kwa ujumla katika bajeti ya mwaka kesho mtaona tunafufua uwepo wa kilimo anga.

Mheshimiwa Naibu Spika, na katika bajeti yetu tukipitishiwa katika Bunge hili tutakuwa tumetenga fedha kwa ajili ya kutumia teknolojia za drones pale ambapo tutahitaji kutumia drones, lakini sasa hivi hatua ya kwanza tuliyochukua, pamoja na kutumia ndege na helikopta tulizonazo ambazo tunazipata kutoka kwenye mashirika mbalimbali ya kimataifa ambayo sisi ni wanachama, lakini kama Serikali tunafanya mazungumzo na taasisi za kimataifa kama World Bank na taasisi nyingine ili tuwe na uwezo wa kutosha na tuwe na ndege zetu za kutosha tuweze kukabiliana na wadudu waharibifu wa mazao.

Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge mtaona kwenye bajeti inayokuja katika Bunge hili, tutakuwa tumetenga fedha yaku-strengthern Kituo cha Kilimo Anga kwa kuwa na vitendea kazi wenyewe badala ya kutegemea vitendeakazi ambavyo tunavipata katika taasisi mbalimbali za kimataifa.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake lakini nina nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, ahadi ya ujenzi wa bwawa na miundombinu ya umwagiliaji kwenye eneo hili ni ya muda mrefu tangu wakati wa Serikali ya Awamu ya Nne. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano aliuhisha ahadi hiyo wakati wa kampeni zake za mwaka 2020. Eneo hili lina maji mengi ambayo yanaleta mafuriko kwenye Kata zaidi ya tano. Kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye majibu yake ni sehemu ya mpango kabambe, swali langu nataka kujua, ni lini ahadi hii itatekelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Wilaya ya Korogwe inaongoza kwa fursa na mazingira mazuri ya kilimo cha umwagiliaji. Serikali haioni sasa ni wakati sahihi kuboresha skimu zilizopo kwenye Tarafa za Magoma na Mombo ikiwemo Skimu ya Kwamkumbo ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri waliitolea ahadi wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu Februari, 2021?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili madogo ya Mheshimiwa Mnzava, Mbunge wa Korogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini tutaijenga Skimu ya Mkomazi, commitment ya Wizara na Serikali ni kwamba katika kipindi cha miaka hii mitano kwa maana ya plan ya 2025, Skimu ya Mkomazi ni moja kati skimu ambazo Serikali itazijenga. Nataka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba hii ni moja kati ya skimu tutakayoipa priority kwa sababu kila mwaka maafa yanayotokea na upotevu wa maji katika eneo hilo ni makubwa sana kuna potential kubwa ambayo na sisi tunafikiri kwamba ni muhimu tukaifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi tuliyoitoa tukiwa katika ziara na Mheshimiwa Waziri Mkuu ipo palepale. Tuliahidi kwamba baada ya mvua hizi wataalam wetu wa Wizara ya Kilimo kwa maana ya wataalam wa Tume ya Umwagiliaji watapeleka vifaa kwa ajili ya kwenda ku-repair ile skimu ambayo ilikuwa imeathirika. Ahadi ile ipo palepale, naomba avumilie, Inshaallah, hivi karibu wataalam wetu watakwenda.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Katika Jimbo la Manyoni Mashariki tuna bwawa la umwagiliaji linalojulikana kama Mbwasa Irrigation scheme. Tayari ilishafanyika upembuzi yakinifu yaani feasibility study zaidi ya miaka 10, tulisaidiwa na watu wa JICA na iligharimu shilingi milioni 200. Napenda kujua sasa commitment ya Serikali ni lini sasa ujenzi wa bwawa hili la umwagiliaji ambalo litasaidia wakulima katika kata zaidi ya tano wa kilimo cha mpunga litaanza kujengwa na Serikali? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tathmini ya mabwawa na maeneo potential mengi ambayo yamefanyiwa usanifu na upembuzi yakinifu kama Wizara sasa hivi tunayafanyia auditing kwa sababu maeneo mengi ukiangalia gharama ambazo zilisanifiwa na hali halisi ya mahitaji ya fedha inayohitajika hazina uwiano.

Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba watupe nafasi katika bajeti tutakapokuja mwaka huu tutatoa mwelekeo wetu wa umwagiliaji clearly ambao kama Serikali tumeamua kwenda nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya eneo ambalo tunalolipa kipaumbele ni kufanya audit kuangalia kweli gharama zinazohitajika katika eneo hili ni halisi na kweli tutapata value for money katika eneo hilo. Njia nyingine ni kwamba miradi mingi ya umwagiliaji tutakayoifanya sasa hivi tutatumia force account na katika bajeti itakayokuja mtaona tutatenga fedha kutokana na Mfuko wa Maendeleo wa Umwagiliaji ambao utakuwa ni chanzo chetu wenyewe kama Wizara bila kutegemea fedha kutoka Hazina katika Mfuko Mkuu. Fedha hizi tutazielekeza katika kununua vifaa ili Tume yetu ya Umwangiliaji iwe na capacity ya kwenda kujenga mabwawa bila kutumia wakandarasi na tutatumia force account kwa kuishirikisha halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge wasubiri, baada ya bajeti tutakuwa tuna mwelekeo sahihi wa sekta yetu ya umwagiliaji.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Skimu ya Pawaga, Ruaha Mbuyuni na Mlalo kule Lushoto tuliahidiwa kwamba zingetengewa fedha baada ya kuharibiwa na mafuriko makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, mpaka sasa ninavyozungumza wenzetu wa Pawaga na Ruaha Mbuyuni wameshapewa fedha lakini sisi milioni 30 ambazo zimeahidiwa na Tume ya Umwagiliaji mpaka sasa hazijafika katika Halmashauri ya Lushoto kwa ajili ya Skimu ya Mlalo. Je, Serikali inatoa commitment gani kwa pesa hizi kwenda katika Skimu hii ya Mlalo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shangazi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Skimu za Mnaro, Pawaga na Ruaha zilikuwa zimeathirika kwa kiwango kikubwa na mvua za mwaka jana na mvua zilizoendelea mwaka huu. Kama Wizara tuliamua kwamba badala ya kupeleka fedha tutumie equipment tulizonazo wenyewe za Tume ya Umwagiliaji na kutupunguzia gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba Skimu za Pawaga na Ruaha zimeshafanyiwa kazi, Skimu inayofuatia kupeleka vifaa ni ya Mlalo ambayo anatoka Mheshimiwa Shangazi na naamini kwamba kabla ya msimu ujao wa mvua tutakuwa tumeshairekebisha na tutatumia vifaa vyetu na Tume watapeleka vifaa wenye kwenda kufanya hiyo kazi badala ya kupeleka fedha. Kwa sababu tukitumia force account tutatumia nusu ya bajeti iliyokuwa imeletwa na halmshari yake.
MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii ya maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa namna ambavyo ametusaidia sana kuchochea zao hili la zabibu, na kupitia yeye wakulima wamehamasika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi sasa ninavyozungumza zabibu zimejaa katika mashamba ya wakulima pale Hombolo, Matumbulu na Mpunguzi na hawana sehemu ya kupeleka. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuhakikisha kwamba zao hilo la zabibu linapata soko la uhakika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali ipo tayari sasa kuwapeleka wataalamu wetu Maafisa Ugani waende kujifunza nje ya nchi namna ambavyo zabibu inalimwa ili kuongeza tija kwa mkulima?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anthony Mavunde Mbunge wa Dodoma Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, cha kwanza hatua tunayochukua sasa hivi, kama Wizara tunaanza utaratibu wa kuweka restriction ya ku-import mchuzi kutoka nje kwa kampuni zinayotumia zabibu ndani ya nchi kabla hawajanunua zabibu yote inayozalishwa ndani ya nchi. Kwa hiyo tutatengeneza utaratibu wa quarter system kwamba aneye-import mchuzi lazima tuone contract zake na wakulima wa ndani; kwamba amenunua zabibu yote na imekuwa exhausted zabibu ya ndani.

Mheshimiwa Spika, kwahiyo tutatumia model kama tunayotumia, ya sukari, ili tuhakikishe kwamba zabibu yetu kwanza inapata soko kama inatumika kwenye wine ama inatumika kwenye vinywaji vikali ili kuhakikisha wakulima zabibu yao yote ina nunuliwa kabla ya kuruhusu kibali cha kuingiza mchuzi kutoka nje. Kwa hiyo huu ni utaratibu na tutaanza nao hivi sasa. Ndani ya siku mbili au tatu zijazo tutakutana na kampuni zote tatu kubwa ambazo ni off taker wa mazao ya zabibu katika nchi ili kutengeneza hii program na kuhakikisha kwamba jambo hili tunalisimamia.

Mheshimiwa Spika, la pili, tunahakikisha sasa kwenda kwenye hatua ya pili. Kwamba badala ya wakulima wa zabibu kuuza tunda waanze kuuza mchuzi. Kwenye hili tumeanza kuongea na wenzetu wa TEMDO Pamoja na wa SIDO ili tuanze kutengeneza centres ambazo wakulima watapeleka zabibu zao. Kama tulivyokwenda pamoja tukiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu tukaona ile pilot ya kile chama cha ushirika cha WAMAKU kilichopo barabara ya Iringa ambacho kinachakata mchuzi na kuuza mchuzi badala ya kuuza zabibu, kwa hiyo hili ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wataalamu sasa hivi wizara tunatambua Maafisa Ugani sita ambao tutawapeleka katika nchi ya South Afrika ili waweze kujifunza; na tunashirikiana na sekta binafsi kwa ajili ya ku-train watu wetu hawa. Na mtaalamu mmoja tuliyenaye nchini, ambaye ni mbobezi ambaye anastaafu hivi karibuni tunafanya mchakato na wenzetu ndani ya Serikali angalau apate extension baada ya kustaafu wakati tuna-train hao wataalamu sita nje ya nchi ili wakirudi tuwe tuna wataalamu wa kutosha wa zabibu.
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na Wizara ya Kilimo; kwa kweli wakulima wa alizeti wameona neema kubwa sana. Hivi tunavyoongea bei ya mbegu ya kilo moja ya alizeti ni 1600, haijawahi kutokea katika nchi yetu. Kutokana na bei hiyo kupanda na kuleta matumaini makubwa sasa muamko umekuwa mkubwa kwa watu kwenda kulima alizeti.

Je, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imejipangaje kutuletea mbegu nyingi za kutosha na za kisasa ili tuweze kulima zao hili kwenye msimu unaokuja hasa kwa Mkoa wetu wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ditopile kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali sasa hivi tumeanza kuchukua mahitaji ya mikoa wanayotuletea wao wenyewe kutokana na uwezo wa mkoa husika katika suala la uzalishaji. Katika mkoa wa Dodoma tunashirikiana kwa karibu kabisa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na RAS ambayo ina-coordinate kutuletea mahitaji ya kila Wilaya ili sisi kama wizara tuweze kuwapatia mbegu. Nataka niwahakikishie wakulima kuwa mwaka huu tutahakikisha wakulima wa alizeti wanapata mbegu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto zilizoko duniani za upatikanaji wa hybrid seed lakini at least tutahakikisha kwamba wakulima wote wanapata angalau standard seed ambazo zitaweza kuwasaidia katika mwaka huu na sisi Serikali wakati huo tunajipanga vizuri kwa ajili ya mwaka mwingine ili tuwe na hybrid za kutosha. Tumeshafanya aggregation tumeshaingia mikataba na wasambazaji na, hivi karibu tutaanza kusambaza mbegu kutokana na mahitaji ya mkoa husika.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nashukuru pia kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, nina maswali madogo ya nyongeza. Kwanza kwa kuwa hali ya maafisa ugani ni mbaya zaidi kwa baadhi ya halmashauri ikiwepo Halmashauri ya Mbulu Mjini na Vijijini ambayo imebakiwa na maafisa kilimo watano tu tangu Mkuu wa Idara hadi vijijini na Halmashauri ya Mji ina maafisa ugani saba tu.

Je, Serikali sasa ina mpango gani kufanya hata reallocation wakati tunasubiria ajira ya Serikali kupeleka maafisa ugani katika maeneo haya?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili mimi naomba commitment ya Serikali kwa mwaka huu wa fedha unaoanza kuweza kuwapeleka maafisa ugani katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu? asante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yustina Arcadius Rahhi Mbunge wa Viti Maalum kwa ufupi sana kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika nimwombe tu kwamba baada ya Vikao vya Bunge hapa tukutane, tutakaa na wataalamu wa wizara, na tutashauriana na wenzetu wa TAMISEMI kuangalia option mbili. Option kwanza kungalia kama kuna uwezekano wa kufanya reallocation; lakini kwa kuwa kuna shortage kubwa tunatumia bodi zetu za mazao kuwaajiri maafisa ugani kwa ajili ya mazao mbalimbali; na Mkoa wa Manyara una advantage kwamba ni moja kati ya mkoa ambao unazalisha zao la pamba. Kwa hiyo tutaitumua bodi yetu ya pamba katika allocation yao ya kuajiri maafisa ugani ili tuone namna gani tunaweza kupeleka maafisa ugani ambao wanaajiriwa na bodi zetu za mazao katika Mkoa wa Manyara na maeneo yenye upungufu.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. kwanza, kwa ruhusa yako, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, alikuja mwenyewe Namtumbo katika kituo hiki na aliona hali halisi ya kituo hiki ambacho Serikali iliwekeza fedha nyingi huko nyuma lakini kilitelekezwa.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza; kwa kuwa Serikali pia ilikiri kwamba kituo kile kina umuhimu wa pekee, hasa kutokana na ikolojia yake, ni kituo pekee kwa Kanda ile ya Nyanda za Juu Kusini. Sasa je, Serikali kwa kuona umuhimu huo, kuanzia sasa inaweza katika mipango yake kuweka fedha za kutosha lakini pia kupeleka wataalam wa kutosha – siyo wanne – wa kutosha, au kushirikiana na mashirika kwa mfumo wa PPP ili kuweza kuzalisha mbegu kwa wingi katika eneo lile?

Mheshimiwa Spika, la pili; kwa kuwa iliyokuwa Taasisi ya Uyole ya Kuzalisha Mbegu wakati ule ilimaliza mgogoro wa ardhi pale kwa kuwaandikia na kuwapatia barua Kijiji cha Suluti kuwakabidhi hekta zao 100. Sasa je, Serikali inaweza kukamilisha taratibu hizo ili wananchi wale pia waweze kulitumia kiuhalali eneo lile kama out growers lakini pia kufanya shughuli zao za maendeleo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Vita Kawawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu kumaliza mgogoro wa hekta 100, mimi na yeye tulikuwa pamoja na niliagiza watu wa TARI na watu wa ASA pamoja na Mkurugenzi wa Maendeleo ya Mazao na halmashauri yake wapime zile hekta 100 ambazo tayari zina makazi ya wananchi na hatuna sababu ya ku-hold eneo ambalo tayari watu wameshajenga hadi nyumba, ni kuichonganisha Serikali. Na nimhakikishie tu kwamba hizo hekta 100 utaratibu utakamilika kama tulivyokubaliana na wananchi watakabidhiwa hizo hekta 100.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kupeleka wataalam na kukifufua, nilihakikishie Bunge lako mwaka huu tunaanza kazi hiyo na tuta-repair majengo na hao watumishi wanne watakuwa ni watumishi watakaoishi palepale, lakini siyo watakaofanya kazi; watashirikiana na Kituo cha Uyole kwa ajili ya kutatua changamoto. Hao ndiyo watakuwa stationed pale mnapopaita SQU kwa umaarufu kule kwenu. Nashukuru. (Makofi)
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kuna sintofahamu kwenye Jimbo langu la Nachingwea kuhusu pembejeo. Wizara ya Kilimo ilitoa tamko kwamba msimu huu wa korosho wakulima hawatakuwa na makato yoyote yatakayokatwa kuhusiana na pembejeo hizo. Hata hivyo, karatasi au fomu wanazosaini wakulima wetu kwenye zile AMCOS inaonekana kwamba kuna makato watakuja kukatwa kwa sababu ya kuchukua hizo pembejeo. Nini tamko la Serikali kuhusu suala hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nimekusoma na nimekuelewa.

Mheshimiwa Spika, labda nirudie tena na niseme kupitia Bunge lako Tukufu kuviambia Vyama vya Ushirika vya Mkoa wa Lindi, Mtwara na Pwani, Serikali ya Awamu ya Sita ya Mama Samia Suluhu Hassan, imetoa ruzuku ya shilingi bilioni 61 kuwapa wakulima wa korosho wa maeneo hayo kwa ajili ya majaribio, asikatwe mkulima yeyote hata senti moja tutakapokwenda kwenye msimu.

Niwaombe Wakuu wa Wilaya wahakikishe kwamba hakuna mkulima yeyote anayesainishwa fomu yoyote ya kuonyesha kwamba anadaiwa hata senti moja. Pia nivitahadharishe Vyama vya Ushirika visijaribu kumkata mkulima shilingi 100, itawagarimu. (Makofi)
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na commitment nzuri ya Serikali ya kuboresha vituo hivi, tunayo changamoto moja kubwa ya Maafisa Ugani wengi wanaopelekwa kwenye baadhi ya maeneo yetu kutokuwa na ujuzi wa kuhudumia mazao ya maeneo husika. Mfano mzuri ni kwenye korosho wapo Maafisa Ugani wanapelekwa wakulima wa korosho wanakuwa wanajua zaidi kuchanganya madawa kuliko hao Maafisa Ugani. Serikali ina mpango gani wa kutumia Vituo hivi vya Utafiti kutoa mafunzo ya ziada kwa Maafisa Ugani wanaowapeleka kwenye maeneo mbalimbali ili wawe na ujuzi wa ziada wa kuhudumia mazao ya maeneo husika badala ya huu ujuzi wanaopewa wa jumla ambapo wakija kule inakuwa ni usumbufu badala ya kuwa msaada.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba kuna gap kubwa ya Maafisa Ugani ambao wanakwenda kuhudumia mazao na aina ya mazao wanayoyahudumia kuhusu suala la uelewa na mabadiliko ya teknolojia imekuwa ni changamoto kubwa sana. Kama Wizara katika programme ambayo tunaianza sasa hivi na mwezi ujao tutaanza training ya kwanza ya Maafisa Ugani 245 wa Ukanda wa Kati na kituo hicho kitakuwa hapahapa Bihawana kwa ajili ya kuwa-training kuhusiana na mazao yaliyoko katika Ukanda huu wa Kati. Kwa ukanda wa maeneo anayetoka Mheshimiwa Nape na yeye mwenyewe nilikuwa naye kwenye ziara hivi karibuni, tumekubaliana mwezi wa 10 kwa kuwa Vyuo vya MATI vinakuwa vimefungwa tutawachukua Maafisa Ugani kutokana na halmashauri husika na ekolojia yake na mazao yanayozalishwa pale na kitu chetu cha TARI Naliendele kitatoa training maalum ya wale Maafisa Ugani kutokana na zao katika eneo husika analotoka Afisa Ugani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nilihakikishie Bunge lako na Watanzania wote kwamba katika mwaka huu wa fedha suala la ku-train Maafisa Ugani ni priority namba moja ya Wizara ya Kilimo. Kwa kuwa bajeti yetu mlishatupitishia sasa hivi wataalam wetu wanaandaa manual za ekolojia tofauti tofauti ili tuanze kazi hiyo ya ku-train Maafisa Ugani as we go on. Nashukuru.
MHE. AHMED ALLY SALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri sana yanayopendeza kuhusu Bwawa la Ishololo. Lakini kwa kuwa tayari andiko lilishafanyika kwa maagizo yake mwenyewe Mheshimiwa Naibu Waziri mwezi nne liko mezani kwake na kwa kuwa mradi huu umechukua muda mrefu na ni muhimu sana kwenye Kata ya Usule Kijiji cha Ushololo na kwa kuwa tayari hapo ameonyesha commitment kwamba 2021/2022 inaweza likajengwa sasa bwawa hili na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ikiendelea kutafuta fedha.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri utakubaliana na mimi kwamba katika mradi huu uwe ni mradi wa kwanza kabisa pale ambapo Tume itakapopata fedha katika mwaka 2021/ 2022?

Mheshimiwa Spika, swali lingine ningependa sana Mheshimiwa Naibu Waziri aweze kutembelea bwawa hili tukienda pamoja ili kuweza kutoa matumaini mapya kwa wananchi wa Kijiji cha Ishololo na Kata ya Usule?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza Mheshimiwa Ahmed Mbunge wa Solwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kwenda kutembelea katika eneo la Ishololo nataka tu nimwahidi kwamba niko tayari na tutakwenda Pamoja. Pili nataka tu nimhakikishie kwamba mradi wa Ishololo, Mradi wa Nyida ambao mradi huu unahusisha vile vile Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini na Nzega District Council kwa maana ya ambayo inahudumia majimbo 3, jimbo la kwake, jimbo la Mheshimiwa Kigwangala na Mheshimiwa Selemani Zedi. Nataka nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba ni miongoni mwa miradi ya priority katika Wizara katika mwaka huu wa fedha na tumeshaanza kufanya visibility study na tutatumia wataalamu wetu wa ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hii fedha ikipatikana.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba niongee kwa uchungu. Wakulima wameuza tumbaku tangu mwezi wa tano mpaka sasa hawajalipwa na wao wanategemea tumbaku ndio waweze kuishi. AMCOS zifuatazo naongea kwa uchungu, AMCA, MISSION, MTAKUJA, IFUTA, TUNAWEZA, KASISI, KATUNGURU, SIPUNGU, MISANGI,
KALEMBERA, BLOKU, JIKOMBOE na UPENDO hawajalipwa hela tangu mwezi wa tano naongea kwa uchungu waishije na sisi tunasema wakulima wanategema kilimo. Lini Serikali itawalipa hawa wakulima ili nao waweze kuendesha maisha yao?

Mheshimiwa Spika, la pili wakati huo bei ya mbolea imefikia hadi laki moja karibu wataanza kutengeneza mabero yao wanafanya nini, hawajalipwa halafu bei ya mbolea imefika mpaka laki moja, naongea kwa uchungu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nimpe pole na nimwambie kwamba kama Serikali tunakiri uwepo wa changamoto hii. La pili ambalo ni vizuri Waheshimiwa Wabunge wakafahamu na yeye ni mmoja kati ya Wabunge ambao mwaka 2019 aliomba Serikali ifanye juhudi za kuhakikisha AMCOS alizozitaja na baadhi ya AMCOS katika Mkoa wa Tabora ambazo hazikuwa na mikataba na ziliachwa na TLTC na ziliachwa na jumla ya tani 12000 ya tumbaku ambazo hazikuwa na wanunuzi.

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara hawa wa kitanzania ndio walio-rescue sector hii na leo tuko confident bei ya tumbaku imetoka dola 1.4 mpaka dola 1.65, zipo changamoto za kuchelewa kulipwa malipo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na niwahakikishie wakulima wa tumbaku moja tutawahakikishia kwamba waliofanya masoko ya mwezi Mei, Juni na Julai tutahakikisha kwamba malipo yao yanafanyika.

Mheshimiwa Spika, la pili tumebadili mfumo wa uuzaji baada ya matokeo ya mwaka jana kwamba makampuni haya sasa tumbaku yao yote wanayochukua kwa wanunuzi haziondoki ndani ya mipaka ya nchi yetu mpaka fedha zimepatikana. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie kwamba hizi changamoto tutaendelea kuzitatua.

Mheshimiwa Spika, kuhusu bei na kuhusu pembejeo sasa hivi wakulima wa tumbaku tumeshaanza kuwapelekea mbole za mabedi bila wao kulipa hata shilingi. Tumetengeneza utaratibu wa suppliers wanapeleka na watalipwa mwisho wa msimu kwa hiyo nataka nimhakikishie kwamba pembejeo zimekwenda.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kupanda kwa bei ya mbolea ni jambo ambalo limetokea na ni kweli nani suala la kidunia. Hatua tuliyochukua mwezi uliopita tumeenda ku- review bei ya tumbaku na wanunuzi wote na kuifikisha dola 1.65 tuki-accommodate ongezeko la bei ya mbolea ili wakulima hawa wasiweze kupata hasara. Nimhakikishie mama Sitta na niwahakikishie wakulima wa tumbaku tumeanza mazungumzo na taasisi za fedha tutahakikisha msimu ujao changamoto ya delay ya payment inakwisha katika sekta ya tumbaku na tutafata sheria ambapo credit facility ni siku 14 na sekta hii iweze kuwa stable.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii niwaulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wakulima wa tumbaku wanalipwa District SES pia wanalipa tozo ile ya Vyama Vikuu vya Ushirika na Chama cha Msingi. Lakini imesikika mwaka huu pia kwamba wakulima wa tumbaku watakatwa na TRA kodi katika mauzo yao ya tumbaku. Nataka kujua Serikali suala hili ni kweli au siyo kweli?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa. Ni kweli Bunge lako tukufu lilipitisha utekelezaji wa Sheria ya Withholding Tax ya 2% kwenye mazao ya kilimo. Lakini kama wizara hatua tuliyochukua kwamba mjengeko wa bei ya tumbaku huamuliwa kati ya mwezi wa pili, tatu na wa nne.

Mheshimiwa Spika, wakati mjengeko wa bei ya mauzo ya mwaka huu yamepitishwa suala la withholding tax halikuwepo. Kama Wizara tumeshawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Fedha tumewaandikia ili tuone namna gani utekelezaji wa sheria hii uweze kuwa withhold kwa sababu mjengeko wa bei haukuhusisha withholding tax ya 2%. Jambo hili liko katika mazungumzo na wenzetu wa Wizara ya Fedha niwahakikishie tu kwamba tutafikia muafaka na kuweza kulinda maslahi ya wakulima katika eneo hili.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali, wananchi wa Jimbo la Kibiti na wajomba zangu wa Rufiji wamekuwa wahanga namba moja sana wa bei za mazao ya Korosho pamoja na Ufuta katika kila msimu katika kila mwaka: Je, Serikali sasa iko tayari kutoa tamko ni msimu gani kutakuwa na mnada wa aina moja katika maeneo yote ambayo yanauza au yanavuna mazao haya?

Swali la pili; bei ya Korosho huwa itegemea sana na…

SPIKA: Hebu rudia swali lako la kwanza.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, Swali langu la kwanza ni kwamba, Serikali iko tayari kutoa tamko kwamba ni lini au msimu upi wataanza kufanya minada inayolingana katika maeneo yote yanayokuwa yanavuna mazao hayo kwa wakati mmoja? Kwa sababu mfumo wa TMX...

SPIKA: Nilisema urudie kwa sababu inaonekana, si ndiyo swali lako la msingi uliuliza?

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, hili halikujibiwa ipasavyo kwa sababu mfumo wa TMX ni mfumo ambao huwa unafanyika kwa kupitia Kanda moja na Kanda nyingine...

SPIKA: Haya endelea.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, Ahsante.

Swali langu la pili: Je, Serikali ina mpango gani; kwa kuwa suala la Korosho huwa linategemea sana na grade ya Korosho; Grade A huwa inauzwa kwa bei ya juu sana, lakini wananchi wa Jimbo la Kibiti pamoja na wajomba zangu wa Rufiji wamekuwa wahanga sana wa bei ya Korosho hasa grade A kwa sababu katika kila msimu Korosho Grade A inayouzwa katika Mkoa wa Pwani bei yake inakuwa chini sana ukilinganisha na Korosho Grade A inayouzwa katika maeneo mengine ambao wanavuna katika msimu unaofanana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kuhusu minada kufanyika kwa wakati mmoja, Waheshimiwa Wabunge watakuwa mashahidi kwamba toka msimu huu umeanza, tumeanza ku-introduce mfumo wa TMX. Mfumo huu umeanza kufanyiwa majaribio katika baadhi ya maeneo na tumeona upungufu wake na tunafanyia marekebisho ili uweze kujenga mazingira ya kuwa na online platform na kuongeza uwazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mfumo wa TMX utakapokuwa umekidhi vigezo tunavyovitarajia, utatumika katika maeneo yote ya kuanzia Pwani, Lindi, Mtwara mpaka Ruvuma ambako kuna uzalishaji wa Korosho lakini minada itaendana na mambo makubwa yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, ya kwanza ni Ikolojia. Kwamba wakati mazao yanazalishwa eneo A na kama eneo B wakati huo huo mazao hayo yamezalishwa, basi minada itafanywa kwa pamoja ili kuongeza transparency.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba sasa hivi timu yetu ya wataalam iko katika
Mkoa wa Pwani ikifanya tathmini kubwa mbili; moja, tatizo la ubora ambalo linasababisha Korosho ya Pwani ikose bei sawa sawa na Korosho ya Tandahimba. Kuhusu suala la changamoto iliyoko katika Mkoa wa Pwani, ambayo Waheshimiwa Wabunge na wenyewe wanaifahamu, kwamba, kwa kuwa Mkoa wa Pwani unakabiliwa na uwepo wa mvua nyingi kuliko maeneo mengine, wakulima wa Pwani wamekuwa wakikumbwa na tatizo la Korosho yao kuwa na unyevu.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Kilimo imeiagiza Bodi ya Korosho sasa hivi kuangalia namna gani tutavisaidia Vyama vya Msingi na Vyama Vikuu vya Ushirika vya Mkoa wa Pwani hasa CORECU ili viweze kuondokana na tatizo la unyevu na kuwapatia vifaa vya kuweza kuanikia Korosho yao ili iweze kukidhi viwango vinavyostahili.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni, wiki ijayo Ijumaa tutakuwa na Mkutano mkubwa utakaoongozwa na Waziri wa Kilimo hapa Dodoma na Waheshimiwa Wabunge wa Korosho tutawaalika, tutagawa vifaa katika baadhi ya Vyama vya Ushirika ili kuongeza ubora wa Korosho katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge watupe muda, tathmini inaendelea na minada itafanyika kwa pamoja. (Makofi)
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa. Kwa kuwa zao la Ufuta katika Mkoa wa Ruvuma linaonekana ni zao linalokua kwa kasi kibiashara: Je, Serikali ipo tayari kutuongezea mbegu na tuwe tunapata mbegu za Ufuta kwa wakati na zilizo bora? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, Wizara ya Kilimo katika Bajeti mtakapoiona itakapokuja, priority yetu ni uzalishaji wa mbegu. Tunataka Mwenyezi Mungu akitujaalia katika Bajeti inayokuja, tuhakikishe nguvu zetu kubwa tunawekeza katika uzalishaji wa mbegu; na Ufuta ni moja ya zao ambalo lipo katika list yetu ya priority na kwa Mkoa wa Ruvuma vile vile zao la Soya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba, Bajeti ya Wizara ya Kilimo itakayokuja katika mwaka ujao wa fedha uwekezaji mkubwa utakuwa ni katika eneo la umwagiliaji na hasa uzalishaji wa mbegu ili tuweze kuondokana na tatizo la mbegu; na Ufuta ni moja ya zao litakalopewa kipaumbele.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020/2025, Chama cha Mapinduzi kiliahidi kwamba Serikali itaweka utaratibu sasa wa kuanza kununua chokocho au mabibo yaliyokaushwa: Je. Serikali iko tayari kuanza kununua mabibo hayo kwa msimu huu wa Korosho unaokuja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ahadi iliyowekwa katika Ilani ni kuhakikisha kwamba mkulima wa Korosho anauza Korosho, anauza Bibo na ikiwezekana hata product ambazo zinatokana na zao la Korosho ikiwemo Siagi na vitu vingine. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie tu kwamba, TARI Naliendele wameshamaliza tathmini ya namna gani ya wakulima wataweza kuvuna Korosho na Ijumaa mkihudhuria kikao mtaona Mheshimiwa Dkt. Kapinga anafanya presentation ya kwanza ya namna ya kuvuna kwa kutumia Neti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatarajia kwamba Serikali haitanunua Mabibo, bali tutahakikisha Mabibo yanavunwa kwa ubora unaostahili ili yaweze kununuliwa na wafanyabiashara na yaweze kuongezewa thamani.

Mheshimiwa Spika, Kongwa vile vile Korosho zako ulizoanza kuvuna hivi karibuni ndani ya kipindi cha miaka hii mitano, Bibo na lenyewe litapata soko. (Makofi)
MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, msimu kwa Korosho unapofika kwenye minada yetu kumekuwa na ubora wa Korosho. Korosho ile ile yenye ubora wa outturn 52 ya Tandahimba, nut-count ya 180 ya Tandahimba, moisture ya 8 ya Tandahimba, inakuwa na bei tofauti na Korosho ya Newala, lakini kila kitu kiko sawa. Je, Serikali inatuambia nini? Kuna nini kati kati yake kinachofanya bei hizi ziwe tofauti wakati ni Korosho zile zile zinazotoka Tandahimba kwenda Newala?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, bahati nzuri Mheshimiwa Katani anafahamu changamoto zilizopo na michezo iliyoko. Nataka tu nimwahidi kwamba, michezo iliyoko na ambayo imekuwepo kwa muda mrefu katika ukanda huo, safari hii tunaenda kuimaliza na tumeanza hatua ya kwanza kwa kuwa na transparency system, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametusaidia sana kwamba minada badala ya kulaza gudulia kesho, kesho kutwa halafu bei ndiyo ifunguliwe, utaratibu huo umeondoka kwa mwaka huu wa kwanza. Mwaka huu tumefanya transparency kwa mara ya kwanza minada hadharani inafunguliwa kwa uwazi.

Mheshimiwa Spika, vile vile tumejifunza jambo jipya. Nataka nimuhakikishie, mbinu za kivita hazitangazwi hadharani, lakini tutalimaliza Mwenyezi Mungu akitujaalia msimu ujao.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa lengo la Serikali ni kuongeza eneo la umwagiliaji kutoka hekta 561,383 ya mwaka 2020 hadi kufikia hekta 1,200,000. Je, Serikali haioni busara kuhakikisha kwamba hii miradi ambayo imeshaanza badala ya kukimbilia kuanzisha miradi mipya tuhakikishe inakamilishwa ili wananchi waweze kuzalisha kwa wingi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mkoa wa Kagera kwa historia yake na jiografia yake ni Mkoa pekee ambao unapakana na nchi nne na nchi hizo nne zina uhaba mkubwa wa ardhi na hivyo uhaba mkubwa wa chakula. Je, Serikali haioni busara kuendeleza hili bonde kuhakikisha kwamba Mkoa wa Kagera sasa unakuwa soko la chakula kwa hizi nchi ambazo zinapakana na Mkoa huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Kikoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kama Wizara priority yetu ya kwanza sasa hivi tunachokifanya na Waheshimiwa Wabunge tutakapokuja kwenye bajeti wataona, ni kufanya tathmini na kukamilisha miradi ya umwagiliaji na tathmini tunazofanya ni za aina mbili; moja kuangalia efficiency ya miradi ya umwagiliaji iliyopo sasa hivi kama inafanya kazi kwa kiwango ambacho kinatarajiwa na kufanya marekebisho pale ambapo tunahitaji kufanya marekebisho. Pia kukamilisha miradi ya umwagiliaji ambayo tumeshaianza. Hatutakuja na mradi mpya wa umwagiliaji isipokuwa kukamilisha miradi tuliyoianza.

Mheshimiwa Naibu Spika, priority ya tatu ni kuwekeza umwagiliaji katika uzalishaji wa mbegu, Serikali ina mashamba 13 ambayo hayana mifumo ya umwagiliaji, mashamba haya 13 ndiyo tutakayoyapa kipaumbele katika bajeti ya mwaka kesho kuwekeza fedha ili yaweze kufanya kazi yote at optimal level ili kuweza kuzalisha mbegu bora na kwa wakati na kuondokana na tatizo la wakulima kutokupata mbegu za uhakika na kuyaacha mashamba idle ambayo hayatumiki. Kwa hiyo hivi ndiyo vipaumbele. Niseme tu ndani ya Bunge kwmaba kipaumbele chetu ni kukamilisha hiyo miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Mto Ngono na umuhimu wa Mkoa wa Kagera, kwetu sisi kama Wizara ya Kilimo na Serikali Mkoa wa Kagera ni moja kati ya mikoa ambayo tunaipa kipaumbele sana na ndiyo tutakapoelekeza nguvu zetu katika kipindi cha miaka mitano. Sababu ya kufanya hivi, mkoa huu strategically umeungana na nchi kama alivyozitaja nne, lakini vile vile ni lango kubwa la kuuza mazao katika nchi ya South Sudan. Kwa hiyo Mto Ngono tutaupa priority kama tulivyosema katika jibu letu la msingi kwamba tunatafuta fedha na tutawekeza katika hizo hekta 11,700 ili waweze kuzalisha mwaka mzima. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Skimu ya umwagiliaji ya Kata ya Ndungu ndiyo skimu kubwa katika Wilaya ya Same na skimu hii sasa inakwenda kufa. Sasa nimembembeleza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa muda mrefu, twende akaione, leo naomba aniambie tunakwenda lini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Malecela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni bahati kubembelezwa na mama. Nikiri kweli Mheshimiwa mama Kilango ameshaniomba twende jimboni kwake na nimhakikishie mama baada ya Bunge hili tutaenda Jimboni kwake pamoja. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza swali la moja la nyongeza. Kwa kuwa Mkoa wa Tanga unazungukwa na milima ya Usambara; na kwa kuwa milima hii inatiririsha maji mwaka mzima hasa wakati wa mvua. Je, Serikali haioni haja sasa ya kujenga mabwawa kuzunguka milima hiyo ili kuchochea kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nikiri mbele ya Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba hatuwezi kutoka katika matatizo ya kilimo bila kuwekeza katika umwagiliaji. Huo ndiyo muelekeo wa Serikali na maelekezo ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Jambo la msingi ambalo tunalifanya sasa hivi kama Wizara kwanza ni kubadilisha modal ya Tume ya Umwagiliaji namna ambavyo inafanya kazi yake; mbili tunachokifanya kama Serikali ili kuweza ku-take advantage ya maeneo kama Milima ya Usambara lakini na maeneo mengine ya nchi yetu kwa ajili ya kujenga mabwawa katika bajeti mwaka kesho mtaona tumeweka chanzo kipya cha fedha kitakachokuwa cha Tume ya Umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tutawekeza kununua vifaa wenyewe ili Tume ya Umwagiliaji iwe na uwezo wa kupeleka vifaa kwa ajili ya kuchimba mabwawa na kujenga miradi ya umwagiliaji yenyewe kwa mfumo wa force account ili kupunguza gharama kubwa tunayotumia katika maeneo ambayo tunajenga skimu za umwagiliaji, kwa sababu gharama tunazotumia ni kubwa na hatuoni value for money. Kwa hiyo tunabadilisha mfumo tutatengeneza mfumo wa force account na tutanunua vifaa wenyewe ambavyo vitakuwa chini ya Tume ya Umwagiliaji kama tulivyofanya katika Skimu ya Pawaga na Ruaha ambako tumetumia vifaa vyetu wenyewe kurekebisha skimu hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge, wasubiri bajeti ya Wizara, wataona mwelekeo wa Wizara katika Sekta ya Umwagiliaji.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kama alivyosema kwenye swali lake alilokuwa akilijibu sasa hivi. Ni kweli ili tuweze kufanikiwa katika kilimo ni lazima tu-invest kwenye kilimo cha umwagiliaji. Mbali na miradi ya Serikali, wananchi katika maeneo mengi wamehamasika kwenye kilimo cha umwagiliaji wakiwepo wananchi wa Bunda, Kata ya Nyatwali ambayo ina maeneo matatu, Nyatwali, Serengeti na Tamau na Mheshimiwa Waziri Mkuu…

NAIBU SPIKA: Swali Mheshimiwa…

MHE. ESTER A. BULAYA: … alishaenda kuutembelea huo mradi mkubwa na akatoa ahadi pale. Kitu kikubwa ambacho…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Ester.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika… ndiyo naenda kwenye swali. Kitu kikubwa wanachohitaji hawana mashine zenye uwezo mkubwa wa kutoa maji ziwani na kuleta kwenye mradi. Sasa, ni lini Serikali au ina mkakati gani wa kuhakikisha wananchi ambao wameamua ku-invest kwenye mradi wa umwagiliaji wanawezeshwa katika vifaa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote. Serikali, hasa Serikali za Mitaa, na tumewaandikia TAMISEMI kuwaomba wa-involve Serikali za Mitaa, maeneo ambayo mnadhani kuna quick wings ambazo tunaweza kuwa na gharama ndogo za uwekezaji na zinahitaji cost ndogo karibuni. Na Mheshimiwa Esther nakukaribisha wizarani njoo tuleteeni andiko kama mnadhani kwamba, kuna mahitaji rahisi ya kuweza kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitumie nafasi hii kuwaomba wakurugenzi wa halmashauri. Suala la umwagiliaji na suala la kilimo sio suala la Wizara ya Kilimo peke yake ni suala ambalo linatuhusu pamoja. Tuwaombe wakurugenzi kwa kuwa, moja ya chanzo cha mapato wanachokipata kinatokana na mazao. Ni lazima asilimia 20 ambayo imeelekezwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu inayotokana na sesi ya mazao wairudishe katika sekta ya kilimo, hasa umwagiliaji na ugani, ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu kuweza kujikwamua katika umasikini. Na sisi Wabunge ni Wajumbe wa Baraza la Madiwani na Kamati za Fedha kwa hiyo, tunaomba tusaidiane katika hili.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika majibu aliyotoa Naibu Waziri, anaeleza mifumo yote ya ununuzi inahusisha kukusanya kahawa katika maghala kwa sababu moja tu ya kuzuia butura. Serikali kushindwa kuzuia butura na kuleta sababu ya kukusanya kupitia maghala ni kutesa wakulima.

SPIKA: Butura ndiyo nini?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, butura ni mfumo ambao wafanyabiashara wanakwenda kwa wakulima kabla ya msimu wanawapa fedha halafu baadaye msimu ukifika wanawapa kahawa.

SPIKA: Ni kama kwenye korosho kangomba.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, sawa. Wamekuwa wakifanya hivyo siyo kwa sababu wanapenda, kwa sababu hela ya kahawa inaletwa ikiwa imechelewa. Sasa nataka niulize swali; ni kwa nini Serikali inapata kigugumizi kuruhusu wafanyabiashara wakanunua moja kwa moja na Serikali ikasimamia kuzuia butura? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama Serikali ikiruhusu KDCU au vyama vya ushirika kukusanya kahawa ije sasa na mkakati wa kuwawezesha kupata fedha ili walipe wakulima mwanzoni mwa msimu kwa sababu inahitajika fedha kwa ajili ya kuandaa mashamba; katikati ya msimu inahitajika fedha kuvuna kahawa na baadaye mwishoni wakiwa wamemaliza kuuza. Nataka nijue Serikali imejipangaje kuhakikisha wakulima wanapata fedha katika awamu tatu na siyo kusubiria baadaye kama wanavyofanya sasa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba iingie tu on record vilevile concern ya Wabunge wote wa Mkoa wa Kagera katika ku- perfect mfumo wa ulipaji ni concern genuine ambayo tunaifanyia kazi kama Serikali. Hata hivyo, niseme kitu kimoja; mfumo wa ushirika ni basic principle ambayo kwanza imeelekezwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, pili, ndiyo mfumo sahihi wa aggregation kwa wakulima wadogowadogo unaoweza kuwalinda. Kwa hiyo, kuondoa mfumo wa ushirika tutakuwa tunatenda dhambi kubwa kabisa ya kuwalinda wakulima wadogowadogo. Tunachotakiwa kufanya ni ku-perfect na tumefanya hivyo katika Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera, Chama cha KDCU na Chama cha KCU katika kipindi cha miaka miwili hii ndiyo vyama pekee ambavyo tumevipatia fedha kupitia Benki ya Maendeleo ya Wakulima kwa riba isiyozidi asilimia tisa. Tunaelewa kuna tatizo la ucheleweshaji wa malipo lakini hatuwezi kufananisha tatizo lililokuwepo miaka miwli iliyopita na msimu huu. Tuwe wakweli na tuseme ukweli mbele ya Mwenyezi Mungu. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wanunuzi kwenda kwa wakulima moja kwa moja; hatumkatalii mfanyabiashara yeyote anayetaka kununua kahawa ya wakulima lakini hatutamruhusu kwenda kumpa mkulima wakati ana shida ya hela kwa shilingi 200 halafu aende akaivune kahawa ikiwa haijakomaa. Wanataka kununua kahawa, waje na leo mimi nina kikao na wewe Mheshimiwa Mbunge nakukaribisha, tutakuwa na kikao cha kahawa tunajadili mfumo na tutawapa leseni mapema. Waseme wazi wanataka kununua kahawa ya wakulima kwa bei gani na volume gani, tutawapeleka kwenye vyama vya msingi lakini direct kwenda shambani hatutaruhusu hilo.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, sababu kubwa inayosababisha wakulima wasipate bei nzuri ya kahawa ni kupeleka kahawa ghafi nje. Serikali ina mpango gani wa kuanzisha viwanda vikubwa ambavyo vitachakata hii kahawa ili kuongeza thamani mkulima aweze kupata bei nzuri ya kahawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatua ya kwanza tunayoichukua specifically kwa Mkoa wa Kagera, sasa hivi kiwanda ambacho kinamilikiwa na wakulima wa Mkoa wa Kagera cha TANICA, installed capacity yao ni tani 3,000. Sasa hivi tunavyoendelea walikuwa wanadaiwa madeni mengi, tumeshachukua hatua ya kwanza kuhakikisha kwamba TADB inafanya intervention kuweza kuyaondoa yale madeni na kuyachukua wao kwa sababu madeni yale walikuwa wanaidawa na benki za kibiashara ambazo zilikuwa zinachaji riba kubwa.

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili, tunakifanyia sasa hivi kiwanda cha TANICA feasibility study ili tuweze ku-expand uwezo wake wa kuchakata kahawa ya wakulima wa Kagera ili kupitia kiwanda chao cha TANICA waweze ku-process na kuuza kahawa iliyochakatwa kama finished product. Vilevile tunafanya maongozi na wafanyabiashara kikiwepo kiwanda kikubwa kilichopo Kagera ambacho kina matatizo na Tanzania Investment Bank ili tuweze kukisaidia kuki-bail out kiwanda kile kiweze na chenyewe kuchakata kahawa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mwelekeo wa Serikali cha kwanza ni ku-perfect mfumo wa soko kuhakikisha wakulima wanalipwa kwanza malipo yao vizuri. Hatua ya pili ni expansion ya TANICA ili Mkoa wa Kagera waweze kuuza kahawa yao ikiwa processed.
MHE. MARIAM D. MZUZURI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, kwanza niipongeze Serikali kupitia Wizara ya Kilimo kwani wamekuwa wanafanya programu nyingi sana za kumwezesha mkulima hasa wa alizeti. Lakini pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mbegu bora ndio ambayo inazalisha zao bora, lakini changamoto kubwa ambayo inawapata wakulima wetu ni upatikanaji wa mbegu bora, lakini tuliona Serikali ikizindua mpango rasmi wa kugawa miche ya korosho kupitia Bodi ya Korosho katika Mikoa ya Kanda ya Kati, lakini sifa kubwa ya mikoa hii hususan Dodoma, Singida, Manyara na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Morogoro ni mikoa ambayo inazalisha alizeti bora sana. (Makofi)

Je, Serikali kwa nini haioni sababu yak ama walivyogawa mikorosho, wawe na programu maalum ya kugawa mbegu bora za alizeti kwa mikoa hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, niipongeze Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, hususan Naibu Waziri wetu Mheshimiwa Hussein Bashe, amekuwa ni msikivu na kutatua changamoto zetu kwa haraka. Wamefuta mfumo wa kuuza mazao kwa mfumo wa TMX ambao kwa kweli ulikuwa kero kubwa sana kwa wakulima wetu, lakini pia hawaoni haja ya kusitisha pia mfumo wa stakabadhi ghalani, hususan kwa mikoa ambayo bado hawana miundombinu na mfumo mzuri kwa ajili ya stakabadhi ghalani?

Mheshimiwa Spika, mfano mzuri hapa Mkoa wetu wa Dodoma, Wilaya za Chemba, Bahi na Kondoa ambao tunazalisha sana ufuta na choroko, hatuna AMCOS, hatuna uongozi wowote. Kwa nini wasitoe muda ili tuweze kujiandaa tuunde mifumo mizuri halafu ndio tuweze kuanza kutumia mfumo huu wa stakabadhi ghalani? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mariam Ditopile wa Mzuzuri.

Mheshimiwa Spika, kwa nini tusigawe mbegu za alizeti kama ambavyo tuligawa miche ya korosho?

Mheshimiwa Spika, sababu ya Serikali kugawa miche ya korosho kwa wakulima katika mikoa ambayo ni mipya ya uzalishaji wa korosho ama michikichi sababu ya kwanza ni zao la korosho na zao la michikichi return on investiment kwa mkulima inachukua muda mrefu sana. Ukiangalia korosho mpaka mkulima aanze kupata mapato ni baada ya miaka mitatu, kwa hiyo, mfumo wa ku-finance input inakuwa kidogo ni gharama kwa mkulima na inakuwa inamuingia gharama nyingi, kwa hiyo, Serikali iliamua kuchukua hiyo hatua, ili kuweza kumpunguzia makali ya kununua miche na kuihudumia kwa kipindi cha miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwenye alizeti hatua ambayo tunachukua kama Serikali nikiri kwamba upatikanaji wa mbegu bora imekuwa ni changamoto na gharama ya mbegu inayopatikana ni kubwa kwa hiyo, mkakati wa Wizara ya Kilimo na mtakuja kuona kwenye bajeti yetu mwaka huu, Inshallah Mungu akijalia, ni kwamba tunawekeza katika mashamba ya Serikali, mifumo ya umwagiliaji. Na kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi kwamba ASA tutawapatia fedha kiasi cha shilingi bilioni 10. Hatua ya kwanza tunayoichukua ni kufanya jitihada na mwaka huu tumeanza kuishusha bei ya mbegu ya alizeti kutoka 35,000 ambayo wanayo sasahivi mpaka angalao shilingi 17,500 kwa kilo mbili kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, nah atua hii tunaifanya kwa kuiwezesha ASA na mwaka huu imefanya pilot project. Imeuza mbegu zake za aina ya OPV ambazo uzalishaji wake wa mafuta hauna tofauti na mbegu ya high breed inayouzwa na kampuni binafsi kwa shilingi 35,000.

Kwa hiyo, tunaamini kwamba, kwa kuisaidia ASA itatusaidia kupatikana mbegu ya kutosha na tutasambaza kwa wakulima na katika bajeti yetu kuna mikoa ambayo ni ya uzalishaji wa alizeti ambayo tutaitaja katika bajeti ambayo tutaifanyia majaribio ya kupata mbegu, lakini vilevile tutaifanyia majaribio ya mifumo ya kusambaza mbegu hizo kwa wakulima, lakini vilevile kuwafanyia majaribio ya end to end contract, ili mkulima kama hana fedha tutengeneze utaratibu utakaomhusisha mnunuzi, mkulima apate mbegu bora na aweze kuzalisha shambani na kumuuzia mnunuzi moja kwa moja.

Kwa hiyo, hatuwezi ku-committ hapa kwamba, tutagawa mbegu za alizeti bure, lakini tunachoweza ku- committ ni upatikanaji wa mbegu za kutosha, lakini vilevile kuishusha bei kutoka 35,000 mpaka 17,500 ama elfu 15 kwa kilo mbili.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mfumo wa stakabadhi ghalani; kwanza ni vizuri nitumie Bunge lako Tukufu ikaeleweka. Stakabadhi ghalani ni maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hili ni jambo la kwanza, lakini la pili stakabadhi ghalani ni mfumo ambao unasaidia kupatikana kwa bei halisi ya zao (price discovery). Ndio lengo la uwepo wa mfumo wa stakabadhi ghalani kwa ajili ya ushindani.

Mheshimiwa Spika, lakini ili uweze kutekeleza mfumo wa stakabadhi ghalani kuna mambo ya msingi ambayo ni lazima yawepo; la kwanza lazima kuwepo kwa chama cha msingi cha ushirika, ili wakulima waweze ku-aggregate, la pili lazima kuwepo na maghala, la tatu lazima kuwepo na wanunuzi ambao watashindana kwa uwazi.

Mheshimiwa Spika, ninakiri kwa niaba ya Serikali na Wizara kwamba yapo maeneo ambayo mfumo wa stakabadhi ghalani una changamoto. Na kama tulivyoamua kustopisha (stop) mfumo wa TMX tutasitisha katika baadhi ya maeneo ya nchi yetu kwa mwaka mmoja wakati tunajenga ushirika imara katika maeneo hayo, lakini maeneo hayo mfano Mkoa wa Dodoma, Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Singida, lakini Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Songwe katika maeneo haya hatuna ushirika imara, kwa hiyo, sasa hivi timu yetu inafanya kazi ya kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nitumie Bunge lako Tukufu kuwaomba Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa na Wakurugenzi katika mikoa hii kwa mwaka huu, hatua ya kwanza wanayotakiwa kufanya wachukue, wasajili wanunuzi wote wa mazao ya ufuta, choroko na, dengu katika maeneo yao na wawapatie leseni bure. Hatua ya pili wazuwie uuzaji wa mazao ya ufuta, choroko na dengu kwa kutumia madebe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi, leo katika Wilaya ya Songwe mkulima anauza debe la kilo 14 kwa shilingi 20,000 ufuta, ambayo ni sawasawa na shilingi 1,400 average per kilogram, huu ni wizi, wakati FOB rate ya ufuta ni shilingi 3,000 katika port ya Dar Es Salaam. Kwa hiyo, tutatoa waraka na maelekezo ya namna ya kufanya, lakini Halmashauri ziwasajili wanunuzi bila kuwa-charge chochote, zianzishe point of sale katika kila kijiji na waweke mizani. Ni marufuku kuuza mazao ya kilimo kwa kutumia madebe na kufunga kwenye lumbesa. Nashukuru. (Makofi)
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nataka kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa kuna umuhimu na mmeshaanza kufanyia kazi suala la Kurasini Logistic Hub kwa ajili ya mazao ya horticulture ili kuweka mfumo huo wa cold chain; Serikali mmejipanga vipi kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kwa sababu, ndiko wakulima wakubwa wa zao hili la parachichi waliko? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kwamba wanaweka mfumo wa ubaridi kwenye reli ya TAZARA ili kuendelea kuwasaidia wakulima hawa kusafirisha parachichi zao kwa bei nafuu kwenda kule Kurasini kwa ajili ya kupelekwa nje kwa kutumia Bandari ya Dar es Salaam; na vilevile kuhakikisha kwamba parachichi zao na mazao mengine ya mbogamboga yanafika yakiwa na ubora?

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna umbali wa kutoka Nyanda za Juu Kusini mpaka Kurasini kule Dar es Salaam kitu ambacho bado kinaweza kukasababisha mazao yale yakakosa ubora: Je, mmejipanga vipi kama Serikali kuhakikisha kwamba mnaweka mfumo wa ubaridi katika mabehewa haya ya TAZARA?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa zao hili limeonyesha linaingiza pato kubwa Tanzania; Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kwamba wakulima wale wanaendelea kulima kwa ubora kwa kuwapelekea mbolea na kuwasimamia katika suala zima la uzalishaji wa zao la parachichi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba zao la parachichi na subsector ya horticulture ni moja kati ya sekta zinazokua kwa kiwango kikubwa na inaajri watu wengi sana hasa vijana, akina mama na middlemen wameanza kwenda katika maeneo haya. Tunafanya nini?

Mheshimiwa Spika, cha kwanza, hivi karibuni Wizara ya kilimo kupitia Waziri wetu, Profesa Mkenda amekutana na representative wa European Business Council kwa ajili ya ku-attract private sector kuja kuwekeza kwenye cold chain ikiwemo mabehewa yenye ma-fridge kwa ajili ya reli ya TAZARA na hata reli yetu kuelekea upande wa Kaskazini kwa sababu ni maeneo ya uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, vilevile pilot katika Wilaya ya Njombe, tumeanzisha centre ya kwanza ambayo imekuwa ni mradi uliofanywa na Wizara ya Kilimo, Tanzania Horticulture Association na Halmashauri ya Njombe kuweka park house ya kwanza ikiwa ya majaribio na imeonesha mafanikio.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa kama Wizara tunaangalia uwezekano wa ku-attract sekta binafsi ili iweze kuwekeza katika maeneo haya ambayo yanakuwa kwa kiwango kikubwa na wengi wameonesha appetite na wamekuja kuongea nasi. Nasi tunatumia Bunge lako Tukufu kuwaomba na kuendelea kuwahamasisha wawekezaji wa Kitanzania waweze kuwekeza. Hata hivyo Kurasini itaunganishwa na Njombe ili tuweze ku-process katika primary level na tuweze kupeleka Kurasini kwa ajili ya kuingiza kwenye meli.

Mheshimiwa Spika, kuhusu tumejipanga vipi kwenye kuwasaidia wakulima; sasa hivi hatua ambayo tunachukua na lilitolewa agizo na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba katika maeneo yote ya uzalishaji hasa ya maeneo ya Nyanda za Juu Kusini, halmashauri zote zimeagizwa zitenge maeneo kwa ajili ya kuzalisha miche ambayo itatumika kuwagawia wakulima.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wakulima wananunua karibu na shilingi 5,000/= kwa mche mmoja, lakini hatua ya pili tuliyochukua kwenye eneo la miche ni kwamba, tumeanza kuwasajili wazalishaji wote wa miche ambao ni wazalishaji wadogo wadogo na kuwaunganisha na kituo chetu cha Uyole ili kuweza ku-protect mbegu ya hasi ambayo ndiyo mbegu yenye thamani kubwa katika soko la dunia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Wizara sasa hivi tunavyomalizia huu mkakati wa kutokea 2021 mpaka 2030, itakuwa ni road map ambayo itaonesha ushiriki wa Serikali, ushiriki wa sekta binafsi na hatua tutakazochukua kwa ajili ya kuhakikisha kwamba sekta hii tunailinda na kuipatia vivutio vyote ili viweze kumsaidia mkulima na kuongeza pato la Taifa. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa zao la parachichi ni zao ambalo linasifika na linaingiza kipato kikubwa kwenye Taifa letu, ni sawa sawa kabisa na zao la nanasi lililoko jimboni kwangu. Zao hili linaonekana kama tunda tu la kuliwa holela holela, lakini ukienda kwenye masoko kama Dubai linauzwa mpaka dola 30 wakati kwetu Usukumani linauzwa shilingi 200/= mpaka shilingi 500/=.

Je, Wizara mmejipangaje kutusaidia wakulima wa mananasi, hasa kwenye Jimbo la Geita Vijijini ili nalo liwe na soko kama soko la parachichi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Mkoa wa Geita ni mmoja kati ya mikoa inayozalisha nanasi na vilevile katika mikoa mingine kama ya Pwani, Wilaya ya Chalinze na Wilaya ya Bagamoyo ni miongoni mwa wilaya zinazozalisha nanasi kwa kiwango kikubwa. Hatua tunayochukua sasa hivi kama Wizara, cha kwanza, ili kuweza ku-meet international standards na mazao yetu ya matunda yaweze kuuzwa katika masoko ya Kimataifa na vilevile yaweze kukidhi mahitaji ya viwanda vyetu vya ndani vya juice; hatua tunayochukua sasa hivi kama Wizara, tumewaagiza TARI ili kuweza kuzalisha mbegu ambazo zitakidhi viwango vya viwanda na kukidhi ubora unaostahili kuweza kumsaidia mkulima.

Mheshimiwa Spika, changamoto tuliyonayo katika subsector ya matunda ya nanasi na machungwa, kwa muda mrefu kumekuwa hakuna uwekezaji wa kutosha tuliofanya kama nchi katika eneo hili kwa sababu lilikuwa halionekani kama ni eneo la kimkakati. Kama Wizara, sasa hivi sekta ya matunda na mbogamboga imepewa kipaumbele kikubwa na tumeagiza TARI Selian kuwa ndiyo kituo halisi kwa ajili ya kufanya research and development.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti yetu Mungu akijalia mwezi ujao mtaona kwamba, uwekezaji tunauweka katika research and development ili mazao ya mananasi na matunda yaweze kukidhi mahitaji ya soko la ndani na soko la Kimataifa na viwanda vyetu viweze kupata matunda wanayostahili.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tuna soko la Shinyanga, Jambo amefungua kiwanda cha ku-process nanasi. Tunamhakikishia Mheshimiwa Musukuma, mimi mwenyewe nitachukua hatua ya kuwaunganisha wakulima wake moja kwa moja waweze kuuza kwa Jambo pale Shinyanga. (Makofi)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, natoa shukrani kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ushirika, ushirika ni kwa wana ushirika wenyewe lakini sasa hivi hali ilivyo ushirika umekuwa ukiwalazimisha watu ambao sio wanachama kwenda kuuza mazao yao kupitia kwenye Vyama vya Ushirika. Serikali ina mpango gani wa kuwaruhusu kampuni binafsi na wafanyabiashara kwenda kununua moja kwa moja kwa wakulima siyo kupitia kwenye ushirika? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa sasa hivi hili ni moja ya mazao ya kimkakati na limekuwa likishuka uzalishaji; kwa mfano takwimu za Mkoa wa Songwe limeshuka, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba wanawakopesha wakulima fedha ili waweze kununua pembejeo kama mbolea na dawa na CPU ili kusudi waweze kuongeza uzalishaji na ubora wa kahawa hapa nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hasunga, mwalimu wangu kama ifuatavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini haturuhusu wafanyabiashara kwenda kwa mkulima mmoja mmoja na Mheshimiwa Mbunge na yeye anafahamu, utafiti na experience imeonyesha kwamba mfumo wa kuwaruhusu wafanyabiashara kwenda kwa mkulima mmoja mmoja hasa wa zao la kahawa umepelekea wakulima wengi hasa kwa upande wa Kagera kupata bei ndogo kwani walikuwa wanauza kahawa yao katika mfumo ambao sio halali kwa shilingi 500 au shilingi 700, mpaka wengine kukopeshwa na mashamba yao kunyang’anywa. Kwa hiyo, mfumo wa ushirika umesaidia kumfanya mkulima wa kahawa kuwa na bargaining power.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo changamoto katika ushirika ambazo hata Mheshimiwa Mbunge anazifahamu na ambazo zinapelekea mapendekezo ya kufanya mabadiliko ya sheria ambapo tunachukua hatua. Mpaka sasa tunaamini kwamba mfumo wa ushirika ndiyo njia sahihi ambayo itamsaidia mkulima mdogo mdogo kuwa na collective bargaining power ambayo itamsaidia kuweza kupata haki yake. Kwa nini wasikopeshwe?

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inawagawia miche bure, lakini ili wakopeshwe lazima wawe na vehicles. Wakulima wa pamba ni mashahidi mfumo wa ushirika ndiyo njia pekee itakayowafanya wakulima waweze kukopeshwa. Tumefanya majaribio, tumeona kwenye zao la pamba mwaka huu wakulima wa pamba wamekopeshwa kupitia ushirika zaidi ya shilingi bilioni 37, wamepatiwa input bila collateral yoyote. Kwa hiyo, kama zipo changamoto specific kwa eneo moja tujadiliane tuweze kuzitatua lakini ku- abandon mfumo ambao umetusaidia kuwapatia wakulima bei nzuri. Tunaamini kwamba wafanyabiashara wanaweza kununua kahawa katika Vyama vya Msingi kwa makubaliano yanayoonesha bei na volume bila kuwaruhusu kwenda kwa mnunuzi mmoja mmoja.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa vile wanawake ndiyo wanaoshughulika sana katika kilimo hiki cha vanila lakini mitaji, elimu na ujuzi wao pia ni mdogo. Je, Serikali ina mpango gani wa kuviwezesha vikundi hivi vya akina mama?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali imefanya tathmini gani ya bei hapa nchini kwetu na nchi za nje? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Maryam, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Serikali ina mkakati gani kuwapatia uwezo wa kifedha vikundi vya akina mama ama wajasiriamali waliopo kwenye zao la vanila na mazao mengine ya kilimo. Kwanza, nitumie nafasi hii kuhamasisha Halmashauri zote za Wilaya ambazo zao la vanila na mazao mengine ya kilimo yanapatikana, ni vizuri asilimia 10 ya kukopesha akina mama na vijana ikaelekezwa kwenye maeneo ya uzalishaji ili kuweza kusaidia mitaji yenye gharama nafuu kwa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tutaendelea kuwasiliana na Serikali za Mitaa ili waweze kutusaidia katika hilo na tumepeleka mapendekezo Wizara ya Fedha namna ya kutumia cess inayopatikana kwenye mazao iweze kurudi kwenye uzalishaji badala ya kufikiria kukopesha bodaboda na vitu vya namna hiyo. Hatua ya pili kuhusu financing, Waziri wa Kilimo hivi karibuni ameunda committee ya kuangalia namna gani tunaweza tukapata mitaji katika sekta ya kilimo ambayo inaendana na sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kipengele cha pili, Taasisi yetu ya Tengeru inaendelea kufanya utafiti ambao utatoa majibu halisi ya bei. Naomba nitumie Bunge hili kusema kwamba maeneo kama ya Mbeya ambapo kuna watu wanapita kuwapotosha wakulima kuwaambia kwamba kilo moja ya vanila ni zaidi ya Sh. 150,000 – Sh. 200,000 sasa hivi katika soko, sio kweli, bei iliyopo sasa hivi haizidi Sh. 20,000 – Sh. 25,000. Kwa hiyo, wasiwapotoshe wakulima kwa kuwapa matumaini ambayo siyo sahihi. Wizara ya Killimo sasa hivi tunafanya tathmini na tutatoa taarifa kwa umma kuwaonesha masoko na bei halali za mazao hayo katika masoko ya nje na masoko ya ndani.
MHE. KABULA E. SHITOBELO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuuliza swali langu la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na hali ya hewa au tabia nchi kwa mwaka huu Kenya haikuzalisha vizuri zao la parachichi, hivyo, wafanyabiashara wengi walikuja Tanzania kwa ajili ya kununua zao hili. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhamasisha wakulima kuongeza kilimo hiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuwahamasisha wakulima wa parachichi sio dhambi kumuuzia Mkenya kwa sababu ni export ambayo tunakwenda kuuza ingawa lengo letu ni kwenda kwenye final markets. Kwa hiyo, tunaendelea kuwahamasisha wauze.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili tunachukua hatua gani kuongeza uzalishaji? Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maagizo kwa Halmashauri zote ambazo mazao ya parachichi yanalimwa kutenga maeneo angalau ya ekari 10 kwa ajili ya kuzalisha miche na kuigawa kwa wakulima. Wizara ya Kilimo imeshaanza kazi hiyo kwa kushirikiana na Serikali za Mitaa, hii ni hatua ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya pili ni kuwatambua wakulima na kuwa register ili mazao yao wanayozalisha yaweze ku-meet international standard na hii project tunafanya pamoja na wenzetu wa FAO ili ku-identify pest. Hatua ya tatu tunafungua masoko. Sasa hivi tunamalizia kufungua soko la South Africa lakini tumeanza negotiation na wenzetu wa China ili tuweze kufungua soko la China na ita-pull yenyewe uzalishaji na wakulima watakwenda sokoni wakiwa na soko la uhakika.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipatia nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza mawili. Katika Skimu ya Umwagiliaji ya Igunga, kumekuwa na wakulima wakichukua mikopo mikubwa kwa riba ya asilimia 18, kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji pale Mwanzugi.

Je, nini mkakati wa Wizara kuwasaidia wakulima hao waweze kupata nafuu katika kilimo hicho? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wakulima wa Mkoa wa Tabora, wamekuwa wakipata mikopo kwa gharama kubwa (kwa dola) katika zao la tumbaku.

Je, nini mkakati wa Serikali kuwasaidia wakulima wa zao la tumbaku kupata pembejeo kama mlivyowasaidia wakulima wa zao la pamba? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Seif Gulamali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri kwamba wakulima katika skimu nyingi za umwagiliaji ikiwemo zilizopo katika Jimbo la Igunga Mjini, lakini maeneo ya Mkoa wa Morogoro, maeneo ya Mbarali, kwa maana ya Mkoa wa Mbeya na maeneo mengine, wamekuwa wakipata financing kutoka katika sekta ya fedha kwa riba zaidi ya asilimia 16 mpaka 20 na zaidi ya hapo na wengine wamekuwa wakipata mikopo kwa gharama ya wastani wa riba ya asilimia 3.5 kwa mwezi, ni gharama kubwa. Tumeshaanza mawasiliano na wenzetu wa Benki Kuu ya Tanzania na hivi karibuni tumekutana MDs wote wa Commercial Banks ili kutengeneza Skimu za financing kwenye sekta ya kilimo ambazo zitakuwa na gharama nafuu na zinaendana na uzalishaji wa sekta ya kilimo. Riba hizi za zaidi ya asilimia 20 kwa mazao ya kilimo, wakulima hawawezi kupata faida kutokana na inputs zao. Kwa hiyo, hili tunalifanyia kazi na hivi karibuni mtasikia taarifa ya Kamati ya Kitaifa iliyoundwa na Waziri wa Kilimo kwa ajili ya kuja na financing models za sekta ya kilimo zinazoendana na sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wakulima wa tumbaku, Wizara ya Kilimo tumechukua hatua na mwaka huu wakulima wa tumbaku hawatoenda kukopa hard cash bank kwa sababu sasa hivi wamekuwa wakikopa fedha kwa dola na wamekuwa wakilipa riba za asilimia 7 mpaka 8 na hizi zimekuwa zikiwasababishia matatizo na wengi kukata tamaa kuendelea na uzalishaji wa tumbaku. Kwa hiyo, tunatengeneza programu na utaratibu ambapo wakulima watapatiwa pembejeo na supplier atapata LC na hao wakulima kupitia AMCOS zao hawatoenda benki kuchukua hard cash kulipia pembejeo, watapata pembejeo na watalipa mwisho wa msimu watakapouza mazao. Hapa transaction itakayokuwepo ni guarantee kati ya Wizara ya Kilimo na taasisi za fedha kuwapa guarantee wakulima wasiweze kwenda kuchukua mikopo ya fedha cash kwa sababu, imekuwa ni mzigo mkubwa. Utaratibu huu tumeufanya kwenye pamba, wakulima wamepata pembejeo bila kwenda kukopa fedha benki na watalipa katika mjengeko wa bei. Hivyo hivyo, tutafanya kwenye korosho na tumbaku.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imekwishafanya upembuzi yakinifu katika Skimu za Tawi na Dirimu zilizoko Wilayani Mbulu. Je, ni lini sasa Serikali itajenga mabwawa ya umwagiliaji katika skimu hizo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yustina, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba skimu hizi zote zimeshafanyiwa upembuzi yakinifu na tumeshajua gharama zake. Tunachokifanya kama Wizara sasa hivi tutakapopitishiwa bajeti mwaka huu tutakuwa tuna Mfuko wetu wa Umwagiliaji na tutatumia force account kwa ajili ya kuweza kuzi-develop skimu hizi na tunatarajia mwaka huu tutakuwa na vifaa vya kutosha. Naomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika Mpango wetu wa miaka mitano miongoni mwa skimu ambazo ziko katika programu mojawapo ni hizo zilizoko katika Mkoa wa Manyara.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Sengerema, naomba kuuliza swali la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mradi katika Bwawa la Nyamterera Katunguru, Sengerema na Mradi wa Bwawa la Isole Kishinda katika Halmashauri ya Wilaya Sengerema. Bwana la Kishinda ilipata shilingi milioni 700 na Bwawa la Nyamterera lilipata shilingi bilioni 1.2 lakini pesa hizi hazijulikani ziliko na haya mabwawa hayajachimbwa. Je, Waziri, anaweza akatueleza namna gani wananchi wa Sengerema tutapataje nafuu kuhusiana na uchimbaji wa mabwawa hayo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tabasam, Mbunge wa Sengerema, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa amesema kwamba mabwawa haya mawili yalipata fedha na hizo fedha hazijulikani zilipo, namwomba tu baada ya kipindi cha maswali na majibu tukutane, tuweze kuongea mimi na yeye aweze kutusaidia hizo information alizonazo na tuweze kuchukua hatua ili kufahamu kama fedha zimepotea ama kumetokea tatizo gani? (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina mvua inayonyesha kwa mwaka mzima na kuharibu miundombinu ya barabara zetu, je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mabwawa hasa maeneo ya Makanya, Mbwei, Garibo Eloi, Kwayi, maeneo ya Kata ya Ubiri ili wananchi wale waweze kulima kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tanga na tukizungumzia kuanzia Wilaya ya Lushoto, Wilaya ya Handeni kuelekea mpaka Muheza ni wilaya ambazo kwetu ni priority kama Wizara ya Kilimo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuanzia mwaka ujao priority yetu ni kutumia resources zetu wenyewe kwa maana ya kujenga mabwawa. Sasa hivi tunafanya comprehensive study ya kuangalia maeneo ambayo tunaweza kujenga mabwawa kwa gharama nafuu. Kwa hiyo, maeneo yake ni miongoni mwa maeneo ambayo tunayapa kipaumbele, avute subira tutayafanyia kazi.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba Serikali inisaidie kutokana na mvua kubwa iliyonyesha na ikasababisha mafuriko makubwa ndani ya Jimbo la Hai na kuharibu skimu nyingi sana zilizoko ndani ya Jimbo la Hai, ikiongozwa na skimu kubwa iliyojengwa na fedha nyingi za Serikali inaitwa Skimu ya Kikafu Chini pamoja na Skimu ya Johari, Mwasha na skimu nyingine ndani ya kata tisa zote zimeharibika pamoja na mifereji. Je, ni lini sasa Serikali itafanya ukarabati wa skimu hizi ikizingatiwa ni kipindi cha kilimo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Saashisha is very committed na kazi kubwa anayofanya kwa ajili ya wananchi wake inaonekana. Jana tumekuwa naye pamoja na Mbunge wa Moshi Vijijini kwa ajili ya kuongelea madhara waliyoyapata wananchi na wakiomba msaada wa chakula na niji-commit kwamba Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Kilimo tunaifanyia kazi issue ya chakula na maafa waliyopata wananchi hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu skimu hizi, hivi tunavyoongea sasa hivi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Prof. Tumbo, yuko Mkoa wa Kilimanjaro, Wilaya ya Hai na maeneo yote yaliyoathirika pamoja na Moshi Vijijini, wakifanya tathmini ya athari ya mafuriko hayo ili tuwe na comprehensive plan. Hatuwezi kusema lini kabla ya technical team yetu kurudi na taarifa ya kuweza kuifanyia kazi lakini tuwaahidi tunaifanyia kazi.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii kuuliza swali moja la nyongeza. Kwanza, nipongeze sana Serikali kupitia kwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Bashe kwa namna alivyoshirikiana na mimi katika sakata la ufuta Wilayani Songwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Songwe kuna Kata ya Mbangala bwawa kubwa lilishajengwa toka mwaka 2017 lakini mpaka leo halijamalizika na hatujapewa fedha kwa ajili ya kulimalizia. Ni lini Serikali itatoa fedha kumalizia ujenzi wa Bwawa la Mbangala? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mulugo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya maeneo ambayo yatapewa kipaumbele katika mwaka wa fedha ujao, pamoja
na kuwekeza katika uzalishaji wa mbegu kwa umwagiliaji ni kukamilisha miradi yote ambayo imefanyika either nusu ama inahitaji repair. Kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote, hatutofanya mradi mpya kabla ya kukamilisha miradi ya zamani na skimu ambazo zina upungufu ili ziweze kuzalisha katika optimal level. Huo ndiyo mwelekeo na ndiyo commitment yetu kwa wananchi.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niulize swali lifuatalo; mafuriko yaliyoikumba Hai na Moshi Vijijini yamelikumba pia Jimbo la Vunjo hususani Skimu za Kahe. Je, Serikali ina mpango gani pia kuhakikisha kwamba Skimu za Kahe nazo zinafanyiwa marekebisho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena, Mkoa wa Kilimanjaro, timu yetu ya wataalam hivi tunavyoongea ikiongozwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo ipo huko. Tunatoa uzito sana athari zilizotokea katika Mkoa wa Kilimanjaro, kwa maana ya Wilaya zote zilizoathirika ikiwemo Jimbo la Mheshimiwa Dkt. Kimei.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie kwamba baada ya ripoti ya tathmini kurudi, skimu zote zitakuwa ni sehemu ya priority. Vilevile athari ambazo wakulima wamezipata ambao tuna uhakika kwamba hawatapata mavuno au chakula mwaka huu, tutatoa kipaumbele kinachostahili na kuweza kutatua hizo changamoto. Kwa hiyo, niwaombe Wabunge wa Mkoa wa Kilimanjaro na hasa wilaya zote zilizoathirika, watuvumilie wakati watu wetu wanaendelea kufanya kazi hii katika maeneo yao. (Makofi)
MHE. BALOZI DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na mikakati yote hii ya Serikali ambayo ni mizuri kuhusiana na soko la mazao ya mahindi bado mahindi ni mengi sana kwa wakulima. Hivi sasa debe la mahindi limefikia Sh.3,000, mahindi yam waka jana wakulima bado wanayo na mwezi Juni tunavuna tena yataungana. Serikali inaweza kuiagiza NFRA waende msimu huu wakaokoe adha hii kwa wakulima kwa kununua mahindi haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la moja la Mheshimiwa Balozi Dkt. Pindi Chana, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba wakulima ama wanunuzi bado wana mazao mengi ya nafaka na wakati huo huo yanakutana na msimu wa mavuno hivi karibuni, huu ni ukweli ambao hauwezi kufichika.

Hata hivyo, sasa hivi hatuwezi kutoa commitment kwamba NFRA waende wakanunue nafaka hizo lakni hatua za awali ambazo tunazichukua na naamini baada ya muda mfupi tutalitatua tatizo la biashara kati ya sisi na nchi ya Kenya ambayo imekuwa ikinunua mazao yetu ya mahindi kwa muda mrefu. Naamini kwamba soko hilo likifunguka litaongeza idadi ya mahindi yanayokwenda nje. Vilevile sasa hivi tuna mazungumzo na wenzetu wa WFP ambao nao wameonesha demand ya kununua mahindi zaidi ya tani kama laki moja na nusu.

Mheshimiwa Spika, lakini hatua nyingine ya msingi ambayo tunachukua kama Wizara ni kwamba tunaongea na wenzetu wa Wizara ya Fedha ili kuruhusu taasisi zetu NFRA na CPB kuruhusiwa kupata vibali ziweze kuchukua fedha katika taasisi za fedha na kununua mazao mengi ya wakulima kwa sababu uwezo wetu wa hifadhi sasa hivi umefika zaidi ya metric tons laki tano na kiwango tunachokihifadhi hakizidi laki moja na nusu.

Kwa hiyo, wakipewa kibali kutoka Wizara ya Fedha wataweza kukopa na kununua mahindi mengi pale ambapo tunakumbana na situation kama hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaeleze Waheshimiwa Wabunge na niwaombe Watanzania wenzangu na wakulima wa nchi hii tunafanyia kazi jambo hili la kuijengea uwezo NFRA na CPB. Wakati huohuo tunaruhusu wafanyabiashara wa Kitanzania, yeyote anayepata soko popote duniani aje Wizara ya Kilimo tutampa kibali bure aweze kwenda kuuza mazao yake bila kuzuiliwa popote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuziomba halmashauri zisizuie mahindi, mpunga au mchele unaouzwa popote nje ya mipaka yetu kwa sababu kufanya hivyo itakuwa ni kutomtendea haki mkulima na wala hatuhitaji ukiritimba wowote kwenye trade ya mazao. (Makofi)
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Tume ya Umwagiliaji imekuwa ikipata shida kubwa sana ya bajeti ili kuweza kuteleza majukumu yake yanayohusiana na skimu za umwagiliaji. Je, Serikali ina mkakati gani endelevu wa kuhakikisha Tume hii ya Umwagiliaji nchini inapata bajeti endelevu na si ya kusuasua kama ilivyo sasa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, soko la ndani pekee haliwezi kuwanufaisha wakulima wa mazao katika skimu ya umwagiliaji. Je, Serikali ina mpango gani madhubuti wa kuhakikisha mazao haya sasa yanayopatikana kwenye hizi skimu za umwagiliaji yanapata masoko nje ya nchi kuliko ilivyo sasa?

Mheshimiwa Spika, nakushuru sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Agnesta, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na upungufu wa rasilimali fedha katika maeneo mbalimbali lakini mkakati ambao Serikali unao na hili lilikuwa ni agizo la Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan alilolitoa mwaka jana akiwa Makamu wa Rais katika Mkoa wa Simiyu ni kuzifanya subsector zilizoko ndani ya sekta ya kilimo kujiendesha. Wizara ya Kilimo hatua ya kwanza ambayo tumechukua na Bunge hili likituidhinishia bajeti, katika mwaka wa fedha ujao tunaanzisha kitu tunaita Irrigation Development Fund (Mfuko wa Kuendeleza Umwagiliaji).

Mheshimiwa Spika, suala la ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji ni wajibu wa Serikali. Serikali inaenda kujenga miundombinu ya umwagiliaji kwenye mashamba ya wananchi wa kawaida. Hivi karibuni tumefanya mradi kwenye skimu tano kwa zaidi ya dola milioni 22 katika Mkoa wa Morogoro, tunatengeneza utaratibu ambao umo kwenye sheria kwamba tunapowekeza katika eneo la umwagiliaji kunakuwa kuna kuzizungusha zile fedha ili zirudi katika Mfuko na ziweze kutumika katika eneo lingine.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo katika bajeti ijayo mtaona tunaanzisha Mfuko wa Umwagiliaji ambao utakuwa sustainable na revolving ambao utawezesha sekta ya umwagiliaji kuwa na uhakika wa fedha. Tunawashukuru wenzetu wa Wizara ya Fedha wameturuhusu part of that fund ziweze kuwa retained na Mfuko na hazitaenda katika Mfuko Mkuu wa Hazina ili tuwe na uhakika wa kuweza kujiendesha.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili katika eneo la umwagiliaji badala ya miradi mingi kuendesha katika mfumo ambao tumekuwa tukiendesha sasa hivi, tunafanya miradi mipya kuanzia mwaka kesho kwa kutumia mfumo wa design and build na kutumia force account kama tunavyojenga shule, zahanati na vituo vya afya katika Halmashauri. Pia tutaiwezesha Tume ya Umwagiliaji kwa kuipatia vifaa ili iweze kufanya miradi yenyewe moja kwa moja badala ya kutegemea njia zingine. Kwa hiyo, hii nadhani itatusaidia sana kupunguza gharama za miradi lakini kuifanya Tume kuwa na uhakika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu soko la mazao, siyo tu mazao yanayotokana na skimu za umwagiliaji, dhana yetu ya umwagiliaji mara nyingi tunaitazama katika mpunga tu, kila ukimsikiliza Mbunge au mtu yeyote anaitazama dhana ya umwagiliaji katika suala la mpunga. Sisi tunafanya jitihada ya kufungua masoko ya mazao yote, sasa hivi tunatumia Balozi zetu na hasa mazao ya nafaka, tunaanza communication na nchi ambazo zina masoko tuweze kujenga bonded warehouses kulekule ili wafanyabishara wetu waweze kupeleka mazao na kuyauzia sokoni badala ya kumsubiri mnunuzi atoke Kongo kuja Dar es Salaam au kuja Tanzania kununua. Kwa hiyo, hii ni njia nyingine ambayo tunaitumia, tunaamini kwa kutumia Mabalozi; kupunguza ukiritimba katika biashara ya mazao; kufungua mipaka; kupunguza gharama za biashara na kuongeza tija mazao yetu yatapata masoko ya uhakika.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika eneo la Zuzu, Jiji la Dodoma kuna bonde kubwa sana ambalo linafaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Je, Serikali haioni umefikia wakati wa kuweka miundombinu katika bonde hili la Zuzu ili kusudi kuendeleza kilimo cha umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mama Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, siyo tu eneo la Zuzu, Wizara ya Kilimo tutatumia potential area zote ambazo tunaweza kwanza kukusanya maji kwa ajili ya mabwawa ambayo yana gharama nafuu, lakini maeneo yote ambayo yana mabonde na yanatatusaidia katika eneo la umwagiliaji na hasa hii mikoa ya kati ambayo ina ukame lakini ina mvua za kipindi kifupi lakini nyingi.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Zuzu na maeneo mengine yote ambayo ni potential katika Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine tutaiweka katika mipango na tutaifanyia kazi.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kama tulivyosikia majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ni kwamba ni hekta 10 tu ndizo zimeendelezwa kwa asilimia 100 na wakati hekta zilizotengwa zaidi ya miaka 10 ni hekta 110. Kwa hiyo inashangaza sana kuona kwamba uendelezaji unasuasua sana. Napenda kujua, ni lini sasa hekta zote 110 zitaendelezwa ili kusudi wapatikane wawekezaji wengi Zaidi kwa sababu mpaka sasa ni wawekezaji watatu tu ndiyo wamepatikana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; nataka kujua kama Serikali sasa itakuwa tayari kutoa sehemu ya eneo kwa ajili ya wajasiriamali wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ili waweze kufuga kuku katika large scale kwa ajili ya ku-export nchi Jirani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Wambura.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza dhamira ya Serikali bado haijabadilika kwa hiyo ku-off load hilo eneo kwa ajili ya matumizi mengine, mahitaji ya namna hiyo yakitokea na ikionekana malengo ya awali yaliyokuwa yametengwa eneo hilo lote kwa ajili ya uwekezaji wa Oil and gas yamekuwa absolute kwamba haliwezi kufanyika then Serikali inaweza kutazama. Mpaka sasa Serikali bado inaamini kwamba kuna umuhimu wa kulihifadhi eneo hilo, kwaajili ya kuendelea kufanya expansion kwa awamu kutokana na mahitaji kama ilivyo sasa hivi. Kwa hiyo suala la kuligawa hilo eneo kwa matumizi mengine hilo bado halina nafasi kwa kipindi hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu lini litaendelezwa lote; kama sote tunavyofahamu kwamba kuna wakati wa biashara ya gas na oil duniani ina-boom na kuna wakati imeshuka. Sasa hivi kama mtaona kwamba malengo yalikuwa ni kufanya uwekezaji kwa ajili ya kuhudumia uwekezaji wa oil and gas katika nchi yetu ya Tanzania, lakini kwa ajili ya nchi ya Msumbiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote tunafahamu kwenye ulimwengu namna gani ambavyo explorations ya gas ilivyoshuka na namna ambavyo uwekezaji uliokuwa ufanyike Msumbiji na wenyewe ume-delay sasa hivi. Kwa hiyo naamini kwamba Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Mtwara, mahitaji ya eneo hilo kwa ajili ya uwekezaji mkubwa kwa ajili ya gas na mafuta bado unahitajika duniani. Kwa hiyo tuta- expand matumizi ya eneo hilo kutokana na demand na kama kuna wawekezaji wako tayari maeneo ya Mtwara na wameshawa-approach Wabunge ama wananchi wa Mkoa wa Mtwara wanakaribishwa Wizara ya Viwanda na Biashara ili tuweze kujadili pamoja namna ya kulitanua hilo eneo.
MHE. ALLY A. JUMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijauliza naomba unipe nafasi pia nikushukuru wewe na Bunge hili tukufu kwa niaba ya Wananchi wa Kyela, pia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuhakikisha kwamba baadhi ya wananchi wanapata msaada hasa wale walioathirika na mafuriko. Naomba niseme ahsante sana kwa Mama yetu Rais wetu ambaye ndiyo anayeongoza nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni kama ifuatavyo; nikweli kuna Scheme ambazo zimetajwa za Ngana na Makwale, hizi skimu zimechukuwa tumito tudogo na tuchache sana ambayo tuna maji machache.

Sasa naomba niulize Serikali je, wanampango gani wa kutumia Mito ya Mbaka, Rufirio na Kiwila, mbali na Songwe ambayo ina maji mengi na ya msimu wote ili kujenga mabwawa makubwa kama ilivyofanyika utafiti na JICA miaka 1969 mpaka 1970 ili pia tupunguze mafuriko?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Kyela tunaelekea kupata mwekezaji mzuri ambaye yuko tayari kuendeleza zaidi ya hekari elfu 10 akishirikiana na wananchi, lakini pia yuko tayari kujenga kiwanda kikubwa ambacho kita-process mpunga. Je, Serikali itakuwa tayari kushirikiana na mwekezaji huyo na sisi kwa Pamoja? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili la mwekezaji, wala halihitaji majadiliano marefu, kama mwekezaji yupo na serious investors karibu Wizara ya Kilimo tukaenaye, tujadiliane naye tuone anahitaji msaada gani ili tuweze kusaidiana kuweza kufikia adhima ya kuwekeza na haya ni maelekezo ya Serikali wala hatutomsumbua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mito miwili aliyoitaja nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge; mfano maeneo yete yaliyokubwa na mafuriko sasa hivi kwa maana kuanzia Mkoa wa Kilimanjaro na maeneo ya Kyela kwa maana ya Mkoa wa Mbeya na maeneo mengine, wataalamu wetu wa Wizara ya Kilimo wapo sasa hivi wameshakwenda kwa ajili ya kufanya tathimini na ingawa kuna stand ya JICA na zipo stand zingine ambazo zilifanywa katika baadhi ya maeneo kwenye nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wataalamu wa Wizara ya Kilimo wa Tume ya Umwagiliaji wana review stand zote zilizofanywa zamani ili kuangalia namna gani tunaweza kuziboresha na kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wengine wote kwamba maeneo yote potation yatafanyiwa kazi katika kipindi cha miaka hii mitano Inshallah!
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza sijaridhika kabisa na majibu yaliyotolewa na Serikali kwa sababu wakati anaongea maneno haya Kiwanda cha TPI tayari mwekezaji aliyeko pale ameshauza ekari tano kwa 1.3 billion kwa mtu mwingine na ukizingatia Serikali ina share ya asilimia 30 kwenye kiwanda hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza, tunafahamu kwamba Serikali ilipeleka kiasi cha dola milioni 10 kwenye Kiwanda cha General Tire. Ningeomba nipate majibu leo hapa fedha hizo zimefanya kazi gani na zimeendeleza nini katika kiwanda hicho ili kiweze kutoa ajira na fursa kwa watu wa Arusha na Watanzania?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali ina mpango gani pia wa kufufua kiwanda chetu cha TPI ili tuweze kuongeza dawa, lakini pia na kuongeza ajira kwa watu wetu wa Arusha na nchi nzima ya Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu Kiwanda cha TPI, asilimia 30 ya kiwanda hicho Serikali ina own share. Kwa hiyo, Serikali iko katika hatua za kutafuta mwekezaji ambaye atawekeza kwa ubia na Serikali, ili kiweze kufufuliwa. Kama Mheshimiwa Mbunge ana mwekezaji yeyote na Bunge hili na Watanzania wote, Kiwanda cha TPI kiko open kwa kumpa mwekezaji kwa kiwango cha asilimia 70 ili kiweze kufunguliwa. Ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba kiwanda hicho kinafunguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Kiwanda cha General Tire, ni kweli Serikali iliweka fedha na ni kweli kwamba mwekezaji aliyekuwa amewekeza eneo lile na aliyekuwa amepewa ownership ya kuki-run kiwanda kile alikabidhiwa fedha na tathmini ya awali ilionesha kwamba fedha zile hazikuweza kufikia malengo yaliyokuwa yametarajiwa. Kwa hiyo, Serikali hatua iliyochukua ni kuhakikisha kwamba kwanza inakirudisha mkononi mwake na kukikabidhi Shirika la NDC kukitafutia mwekezaji mwingine. Yule bwana aliyekuwa amepewa majority shareholder share zake zilirudishwa Serikalini. Kwa hiyo, ni dhamira ya Serikali kuona kwamba Kiwanda cha General Tyre kinafanya kazi ili kufikia lengo la Serikali kwa ajili ya kuwekeza katika eneo hilo.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa swali hili linalohusiana na Kiwanda cha General Tyre limeulizwa kwa muda mrefu sana na sisi tumekuwa tukifuatilia muda mrefu sana tangu Mheshimiwa Gambo akiwa Mkuu wa Wilaya, amekuwa Mkuu wa Mkoa, hadi leo hii yupo ndani ya Bunge, lakini Serikali imekuwa ikitoa majibu yaleyale. Wananchi wa Arusha wanataka kufahamu ni lini Kiwanda cha General Tyre kitaanza kufanya kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA
NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Serikali dhamira tunaelewa na frustration iliyoko kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha na umuhimu wa Kiwanda cha General Tyre. Hili jambo ni la wazi, ni dhamira ya Serikali kuona kwamba Kiwanda cha General Tyre kinafanya kazi. Ndiyo maana Serikali mara zote imekuwa ikitangaza nia ya kumtafuta mwekezaji yeyote mwenye uwezo wa kuwekeza na kuwapa fursa wananchi wa Mkoa wa Arusha na Tanzania kwa ujumla waweze kuwekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni muhimu vilevile Waheshimiwa Wabunge wakaelewa, unapowekeza katika kiwanda kuna dhana ya comparative advantage. Hii ina maana kwamba tunapotengeneza tairi Tanzania, tairi hilohilo linazalishwa na nchi nyingine, tunapoenda sokoni litanunuliwa kwa bei gani? Kwa hiyo, suala la teknolojia ni muhimu sana. Nitumie nafasi hii kuwahamasisha Watanzania kwamba Serikali iko open kumruhusu Mtanzania yeyote mwenye uwezo ama mwekezaji kutoka nje kuja kuendesha kiwanda hiki. Mkoa wa Arusha unakaribishwa kama kuna uwezekano tunaweza kukutana nao kama Serikali tujadiliane ni namna gani tunaweza ku-revive Kiwanda cha General Tyre. Pia siyo lazima kizalishe matairi tu, kinaweza kuzalisha jambo lingine lolote ambalo litaweza kuleta manufaa katika nchi na uchumi.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi. Kwa kuwa, uwepo wa viwanda visivyofanya kazi katika Mkoa wa Arusha inafanana kabisa na Mkoa wa Mtwara ambako kuna viwanda vya korosho ambavyo havifanyi kazi. Naomba kujua ni lini Serikali itahakikisha Viwanda vya Kubangua Korosho vilivyopo katika Mkoa wa Mtwara, Wilaya ya Masasi, Newala na Mtwara vinaanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hokororo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwa muda mrefu Viwanda vya Kubangua Korosho katika Mkoa wa Mtwara na maeneo ya Pwani vilisimama kufanya uzalishaji. Sababu ya msingi ilikuwa ni kwamba mfumo wa uuzaji wa korosho wa minada ulikuwa unawaweka kwenye disadvantage processors wa viwanda ndani ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatua ya kwanza ambayo Serikali imechukua na marekebisho haya tumeyafanya mwaka jana ni kwamba, tumeruhusu mfumo wa primary market kwamba wenye viwanda vya kuzalisha korosho wanaainisha mahitaji yao ya awali na tunawaruhusu kwenda kununua moja kwa moja katika vyama vya msingi badala ya kusubiri kwenye mnada kwa sababu, kwenye mnada wanakuwa not competitive na matokeo yake gharama ya wao kuchakata korosho inakuwa kubwa. Mwaka huu vipo viwanda viwili ambavyo vimeanza kufanya hiyo process na tumevifanyia majaribio na tumeona manufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini changamoto ya pili inayowakabili wenye viwanda vya kuchakata korosho ni thamani ya mtaji unaotakiwa kununua sokoni ili aweze kuhifadhi kwa msimu mrefu kwa maana ya mwaka mzima.

Kwa hiyo, sasa hivi tunafanya mazungumzo na Tanzania Agricultural Development Bank ili tuanzishe mfumo wa Collateral Management System kwamba wenye viwanda wanapata raw material zinahifadhiwa katika maghala, wanakuwa wanachukua kidogokidogo kutokana na mahitaji yao ili waweze ku-sustain katika kipindi cha mwaka mzima. Msimu huu wa korosho utakaoanza mfumo wa primary market kwa viwanda kununua moja kwa moja katika vyama vya msingi tutawaruhusu ili viwanda vya Mkoa wa Mtwara na Lindi viweze kufanya kazi.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naipongeza Serikali kwa kutoa pembejeo bure na mbegu bure za pamba. Imeleta motisha kwa wakulima. Hongera sana Mheshimiwa Bashe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali ya nyongeza mawili. Kwa kuwa, mwaka jana AMCOS imechelewesha sana malipo ya wakulima na mpaka sasa…

SPIKA: Waheshimiwa, naomba sauti zenu mzipunguze tumsikilize Mbunge.

MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, niulize maswali mawili sasa. Kwa kuwa AMCOS, mwaka jana imechelewesha sana malipo ya wakulima na mpaka sasa kuna baadhi ya wakulima wanadai. Serikali haioni sasa umuhimu wa kuwarudisha wakulima kwenye soko huria ili wauze pamba walipwe cash? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali ikiwaruhusu wanunuzi ma- dealers kuingia sokoni moja kwa moja hiyo itasaidia wakulima kwenda kuuza pamba na kulipwa cash halafu itawasaidia vijana wengi kupata ajira kwa vile kuna ukosefu wa ajira. Je, ni nini tamko la Serikali kuhusu kuingia kwenye mfumo wa manunuzi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza mfumo wa ushirika ni takwa la Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Hii ni ahadi ambayo wananchi walikichagua Chama Cha Mapinduzi kuhakikisha kwamba tunajenga ushirika. Hili ni jambo la kwanza. Jambo la pili, ushirika ndiyo njia sahihi ya wakulima wadogo wadogo kufanya aggregation na kwa kutumia ushirika kama alivyosema kwamba tumegawa dawa bure, tumegawa pembejeo bure, tumetumia ushirika kufanya namna hiyo. Kwa hiyo, ziko changamoto kama alizosema Mheshimiwa Mbunge. Utafiti umeonesha kwamba kwenye Sekta ya Kilimo ambayo wakulima wake ni wadogo wadogo, tunapoondoa mfumo wa ushirika hasa katika haya mazao makubwa, mara nyingi wakulima hudhulumiwa na wanunuzi. Kwa hiyo, tutatatua changamoto zilizopo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu AMCOS ambazo hazijalipa wakulima kama wapo tuletewe majina tuchukue hatua. Hili ni jambo la kwanza na kutokumlipa mkulima ni uhujumu uchumi, wako ambao tumeshawafunga. Kuhusu namna gani tunalipa, tumekaa kikao cha wadau wa pamba, tumekubaliana na nitumie Bunge lako kuagiza mambo yafuatayo kwa kuwa msimu wa pamba tunaanza sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, wanunuzi wanaruhusiwa kupeleka ma-cashier wao katika vyama vya msingi na waende na fedha wawalipe moja kwa moja wakulima pale pale kwenye chama cha msingi mahali ambapo hakuna mfumo wa kulipia benki. Hili la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, chama cha msingi ushuru wake utalipwa kupitia benki na wala hautaenda cash kwenye chama cha msingi. Lakini tunaruhusu mifumo yote mitatu. Mnunuzi anaruhusiwa kupeleka walipaji wake kwenye chama cha msingi. Kama chama cha msingi A, kuna makampuni matano, makampuni matano yapeleke ma- cashier wao pale pale ili mkulima anapofikisha pamba yake alipwe cash aondoke na fedha yake na pamba isiondoke kwenye cham acha msingi bila mkulima kupewa fedha yake.

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuua mfumo wa ushirika katika hatua hii. Hili ni takwa la kikatiba na tuna sheria ya ushirika. Kama tuna nia ya kuufuta ushirika katika nchi iletwe sheria na Bunge hili hili likiifuta sisi wizara tutaufuta ushirika bila matatizo yoyote. (Makofi)
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Wilaya ya Hanang wanategemea sana kilimo katika masuala mazima ya uchumi. Lakini katika kilimo hiki tunategemea sana shamba letu kubwa, shamba la NAFCO ambalo kwa sasa lina mwekezaji. Shamba lile lina hekari takriban 40,000. Mwekezaji analima asilimia 20 na eneo analoliacha wazi anawanyanyasa sana wananchi. Je, Serikali inatuambia nini juu ya kurudisha shamba lile Serikalini au kuwagawia wananchi ili tuweze kuingiza kipato katika Serikali na kwa mwananchi mmoja mmoja. Ahsante sana kwa kunipatia nafasi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Halamga na Mheshimiwa Mbunge wa Hanang kwa ufuatiliaji wa eneo ambalo lilibinafsishwa kwa Kampuni ya Ngano Limited. Lile eneo kwa mujibu wa sheria alibinafsishiwa huyu bwana na alilinunua. Sisi kama Wizara ya Kilimo pamoja na Waziri wa Kilimo tumekutana naye na wawakilishi wake na tumefanya nao mkutano. Tumewapa ultimatum ya mwaka mmoja na wao wanafahamu kwamba wasipotekeleza makubaliano tuliyofanya na wao, Serikali itachukua hatua ambazo tumekubaliana nao wao. Kwa hiyo, tuwaombe wananchi wa Wilaya ya Hanang kuweni na Subira. Tumeanza safari ya ngano pamoja na mmeona matokeo na sasa tuwaahidi, tatizo la ngano limited linaenda kuisha.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali lililoulizwa namba 211 linafanana kabisa na wakulima wa Mkoa wa Kagera wanaolima kahawa. Je, Serikali inatoa kauli gani kwa wanunuzi wanaotaka kununua Kahawa kwenye vyama vya msingi. Je, inaruhusiwa? Nilikuwa napenda tamko kutoka kwa Serikali. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, vile vile jambo hili limekuwa likifuatiliwa kwa karibu na Mheshimiwa Innocent Bilakwate na Mheshimiwa Innocent Bashungwa. Naomba nisitoe kauli na hii kauli vyama vya ushirika wa Mkoa wa Kagera kwa maana ya KDCU na KCU. Niseme tu kwamba wanunuzi binafsi, soko la kununua kahawa, soko la kununua mazao yaliyoko kwenye vyama vya ushirika ni masoko huria. Wanunuzi wanaruhusiwa kwenda kuingia mikataba na vyama vya msingi.

Mheshimiwa Spika, na nitumie kauli hii kuwaagiza KDCU na KCU wasimzuie mnunuzi yeyote anayetaka kununua kahawa moja kwa moja kwenye chama cha msingi na wala wasiwatishe viongozi wa vyama vya msingi kuwazuia kuingia mikataba na wanunuzi. Mnunuzi aseme bei anayonunulia na kiwango anachonunulia na wawaruhusu kushindania katika AMCOS level na wasiwachaji tozo zinazohusiana na union kama mnunuzi anaenda kununua kwenye chama cha msingi. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza swali la kwanza nilitaka kujua tu kwa kuwa Mkoa wa Mara ardhi yake ina hali ya hewa nzuri ya zao la Alizeti, na hasa katika tarafa ya Chamriyo Wilaya ya Bunda yenye vijiji 30 na kata saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini sasa Serikali kwakuwa inataka kupunguza uhaba wa mafuta ya kula hapa Tanzania ni lini itapiga kambi pale kwenye Tarafa ya Chamriyo yenye vijiji 30 na kata saba yenye hali ya hewa nzuri ya kulima Alizeti ili kuwapa mbegu bora za kulima Alizeti na kupunguza uhaba wa mafuta hapa Tanzania?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kwa kuwa katika swali lako la msingi umezungumza kwamba Maafisa ugani watapewa pikipiki na vitendea kazi vingine Je, kwa Mkoa wa Mara ambao upo tayari kulima Alizeti ni lini vitendea kazi hivi navyo vitafika kwa maafisa ugani wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza maeneo yote ambayo yana-potential ya kuzalisha Alizeti au mazao yote ambayo yatatusaidia kupunguza tatizo la mafuta tutayapa kipaumbele kama Serikali, na nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge tunaweza kukaa mimi na yeye na tukajadiliana namna gani tunaweza kuanzisha mfumo wa Block farm katika Wilaya ya Bunda, na kwasababu wenyewe wanazalisha pamba, na pamba ni moja ya zao ambalo tunalipa kipaumbele. Kuhusu vitendea kazi ni kwamba kwanza bahati nzuri Mheshimiwa Mbunge anatoka kwenye ukanda wa Pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia bodi ya pamba sasa hivi tumeanza program ya kuwapatia Maafisa Ugani Elimu na vitendea kazi kwenye ukanda wote unaozalisha pamba na Bunda ni moja wa Wilaya na hivi sasa tunavyoongea bodi ya pamba imeanza kukutana na Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Wilaya zinazozalisha pamba ili maafisa Ugani waingizwe kwenye program ya kupatiwa vitendea kazi lakini vile vile kupatiwa vifaa soil analysis kit ambazo watatumia kuwa wanapima afya ya udongo katika maeneo hayo. Kwa hiyo, Wilaya ya Bunda na Mkoa wa Mara ni moja ya Mkoa ambayo kwetu ni potential na tutaipa kipaumbele.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuwa kati ya vikwazo vya zao la alizeti ni upatikanaji mdogo kwenye Mbegu ya alizeti wa mafuta. Je, Serikali haioni haja sasa ya kuja na utafiti wa kina wa kuhakikisha tunapata mbegu bora zinazotoa mafuta kwa wingi ili kuchochea wasindikaji na wakulima wa zao hili la alizeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza utafiti ni jambo ongoing tunaendelea kufanya utafiti lakini tumeshafanya utafiti wa kutambua aina gani za mbegu, tunazo mbegu aina mbili tuna high hybrid na tuna mbegu za OPV ambazo zinatumika kwenye uzalishaji wa alizeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachokifanya sasa hivi kama mlivyosikia kwenye jibu letu la msingi kwamba mwaka ujao wa fedha tutawekeza kiasi cha shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kuzalisha mbegu za kutosha na malengo yetu ni kuzalisha metric tons 5,000 za Mbegu ambazo zitakwenda shambani ambazo zitatupatia metric tons 625,000 za mbegu za kwenda kukamuliwa ambazo zitatupatia metric tons 170,000 za mafuta kupunguza gape yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala la uzalishaji wa mbegu tayari tunashirikiana na sekta binafsi tutazalisha mbegu za kutosha katika mwaka ujao wa fedha na hii itatufanya kwamba tutakuwa tumepunguza 50% ya gape yetu, na mwaka unaofuatia nadhani kwamba tutakuwa tumemaliza. Kwasababu mahitaji yetu ni kupata mbegu za kwenda kiwandani kukamuliwa metric tons 1,226,000 ambazo zitatupatia wastani wa tani 400,000 za mafuta ili tuweze kupunguza kabisa tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na sisi tunaamini kwamba kutoka upande wa Serikali ni kwamba ndani ya miaka miwili au miaka miwili ya fedha tutakuwa tumelipunguza tatizo hili la mafuta kwa kiwango kikubwa na priority ni zao la Alizeti yakifuatiwa na mazao mengine, kwa hiyo, utafiti umeshafanyika na mwakani tunaanza uzalishaji. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto wanazokabiliana Maafisa Ugani mbali na kwamba hawana vifaa, mbali na kwamba wapo wachache lakini wengi hawana ujuzi wa kukabiliana na mazingira ya kisasa. Na tafiti mbalimbali za Serikali zimeonesha kwamba asilimia zaidi ya 90 ya Maafisa Ugani wanatumia zile skills ambazo walikuwa wamepewa shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilitaka Mheshimiwa Naibu Waziri aniambie ni lini basi Serikali itakuwa na mkakati madhubuti wa mafunzo ya maafisa Ugani wetu ili waendane na mazingira ya sasa ya ushindani wa Kilimo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa muda mrefu maafisa ugani wetu kuna gape kati ya technology advancement na elimu waliyonayo. Kwa hiyo, kama Wizara hatua ya kwanza tuliyochukua na mtaiona katika Mpango wetu wa bajeti mwaka huu ni pamoja na kuwapatia vitendea kazi, tutawapatia soil kit kila Afisa ugani ambaye anafanyia kazi katika eneo lake, tutampatia pikipiki lakini training ambayo tutaifanya, tutafanya training ya darasani kwa ajili ya kuwa-equip na technology na knowledge za sasa hivi kutokana na mazao na ecology ya eneo ambalo anafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile kila afisa ugani atakuwa na shamba darasa yeye mweyewe ambalo yeye Afisa Ugani atalisimamia lile Ushamba katika eneo lake kutokana na zao linalozalishwa pale ili liwe ni sehemu ya kufundisha wakulima na gharama za uwekezaji zitatolewa na Serikali katika eneo hilo kwa kumwezesha mbegu, kumwezesha madawa na kumwezesha… ili kuwe kuna- practical experience ambayo wakulima wanaiona na yeye mwenyewe anai-practice kwa hiyo, training ni sehemu ya muhimu na tumeanza repair ya chuo chetu cha Bihawana hapa sasa hivi ambacho kitatumika kwa ajili ya kuwafundisha Maafisa Ugani continues kutokana na mahitaji ya soko na dunia.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante. Naomba sasa kwa kuwa bei ya kahawa kwenye soko la dunia kwa kilo moja inaenda takribani shilingi 9,660 lakini mkulima ambaye anakwenda kuuza kahawa yake kupitia Vyama vya Ushirika kilo moja ananunua kwa shilingi 2,000 bila bakaa.

Je, Serikali haioni iko haja ya kutoa au kuondosha au kupunguza tozo zinazotokana na zao la kahawa ili mwananchi yule ambaye ni mkulima aweze kunufanika na bei hii ya kahawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, Lakini swali la pili, kwa kuwa sasa wananchi wa Jimbo la Hai wako tayari kulima kahawa. Je, Serikali ipo tayari kusambaza pembejeo kwa bei ambayo ni Rafiki kwa wakulima? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ni kweli leo katika soko la dunia kwa bei ya mpaka jana wastani wa Arabica ilikuwa ni Dola 3 wakati wastani wa Robusta ilikuwa Dola 1.5. Na sisi kama wizara na Serikali tumeanza kupitia mjengeko wa bei ambao unahusisha tozo mbalimbali na leo mimi binafsi nitaongoza kikao kitakachohusisha Vyama vya Ushirika hasa vya Mkoa wa Kagera ndio tunaanza navyo. Kwa hiyo, hili la kwamba kuangalia suala la tozo wanazotozwa wakulima katika bei tutalipitia ili wakulima waweze ku-benefits na bei na zao lao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu pembejeo, Serikali sasa hivi inachukua hatua njia pekee ya kuwasaidia wakulima wadogo wadogo ni kupitia ushirika. Tumefanya majaribio katika sekta ya pamba tumeona wakulima wamepata pembejeo za kutosha katika msimu uliopita kupitia Vyama vya Ushirika. Tumefanya majaribio katika tumbaku, wakulima wamepunguza gharama za pembejeo kwa zaidi ya asilimia 40 kwasababu zinanunuliwa in bulk badala ya mkulima mmoja mmoja kwenda sokoni kununua. Kwa hiyo tunajenga Vyama vya Ushirika na nimuahidi Mheshimiwa Mbunge na niwaahidi Waheshimiwa Wabunge wote kwamba tutaangalia njia bora ya wakulima wa zao la Kahawai li Ushirika wao uweze kuwa imara waweze kupata pembejeo katika mfumo wa bulk na waweze kuzinunua kwa bei competitive ya soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakiri mkulima mmoja mmoja kwenda dukani kununua pembejeo moja moja gharama yake inakuwa ni kubwa na wengi wanashindwa kuhudumia mazao. Kwa hiyo, tupokee wazo la Mheshimiwa Mbunge tutatafuta mechanism sahihi ya kuwahudumia wakuliwa wa Kilimanjaro kupitia ushirika wao waweze kununua pembejeo kwa pamoja na hiyo itawapunguzia gharama.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa swali la nyongeza. Wilaya ya Mbinga ni mojawapo ya wilaya zinalima zao la kahawa kwa wingi lakini Vyama vya Ushirika vimekuwa vikichelewesha malipo na hivyo wakulima kushindwa kununua pembejeo za kuhudumia mazao yao kwa wakati.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha utendaji kazi wa vyama vya ushirika ili wananchi wa Wilaya ya Mbinga waweze kulipwa fedha kwa wakati na hivyo kuwawezesha kununua pembejeo za kuhudumia zao lao kahawa kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto kwasababu mfumo wa ulipaji siku zote umekuwa ni kwamba baada ya mnada fedha zinalipwa kwenye Chama Kikuu cha Ushirika, Chama Kikuu cha Ushirika kina hamishia fedha katika Chama cha Msingi. Kwa hiyo tumefanya kikao mwezi Aprili na Vyama vya Ushirika vya Mkoa wa Ruvuma kwa maana ya Wilaya ya Mbinga, utaratibu tunaoelekea sasa hivi kuutekeleza katika vyama vya msingi na vyama vikuu vya ushirika ni kwamba mnada unapoisha mnunuzi anatakiwa alipe malipo ndani ya saa 48 na malipo yale yatakwenda moja kwa moja kwa mkulima hayatopitia kwenye ukiritimba wa kwenda kwenye chama kikuu chama kikuu kwenda kwenda kwenye chama cha msingi. Kwa hiyo nimuahidi Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine tuna-perfect system ya kulipa baada yam nada malipo yaende moja kwa moja kwa mkulima badala ya kupitia kwenye vyama kwasababu huko kunaleta ukiritimba na kuchelewesha malipo.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante sana kwa kunipa fursa. Shirika la Utafiti wa Kahawa Tanzania Coffee Research Institute limezalisha aina chotara za kahawa ambazo huwa huzaa mara tano zaidi ya zile kahawa za asili zilizokuwa zinaitwa Kent. Wakulima wengi wanalima hizi kahawa za zamani ni lini Serikali itaanzisha program maalum ya kuwafundisha wakulima umuhimu wa hizi kahawa mpya chotara kutoka Lyamungo ili waweze kuongeza tija? Wanahitaji mafunzo sana. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Moshi Vijijini na kwa niaba ya Serikali na Wizara ya Kilimo ni-acknowledge kazi aliyoifanya katika sekta ya kilimo akiwa bado chuoni. Ni kwamba Serikali imekwisha anza kazi na tumeanza kuwatumia wataalam wetu wa TaCRI na tumeshaanza multiplication ya miche la kisasa ambayo tunaanza kuipeleka kwa wakulima. Tumeanza kuigawa miche hii kwa baadhi ya wakulima na kuwapa elimu. Kwa hiyo program hiyo imeshaanza na elimu imeshaanza kutolewa kwa wakulima umuhimu wa kwenda kwenye hybrid ili waweze kuongeza mapato yao.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa changamoto ambazo zinakabili zao hili la kahawa katika Jimbo la Hai zinafanana pia changamoto ambazo zinakabili wakuliwa katika Jimbo letu la Kigoma Kaskazini. Ukiangalia moja wapo ya changamoto ni soko na mkulima kuwa na uhuru wa zao hili kahawa kuuza anapotaka. Vyama hivi vya Ushirika vinawafunga wakuliwa wetu, hawawezi kuuza kahawa zao endapo mnunuzi huru atafika katika maeneo husika. Je Serikali inaweza kutupa tamko leo juu ya hilo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni vizuri Waheshimiwa Wabunge tukaelewa kwamba kuna miss conception juu dhana ya ushirika. Ushirika haumzuii mnunuzi binafsi kwenda kununua zao la mkulima. Ushirika ni mfumo wa wakulima wanaokusanya zao lao pamoja na wakulima wale wanauza kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, experience imeonesha kwamba pale ambapo kunakuwa hakuna mfumo wa ushirika hasa katika mazao haya kama kahawa, pamba, korosho na mazao mengine yote wakulima wamekuwa wakiuza zao lao bei ndogo sana. Kesi iliyoko Kigoma Kaskazini na Mheshimiwa Mbunge tumeongea naye mimi zaidi ya moja mara mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema kama kuna mnunuzi binafsi anataka kununua zao la mkulima hasa kahawa, hasa Kigoma Kaskazini na wewe mwenyewe nimekwisha kwambia mlete tutamruhusu atakwenda kununua kwenye Chama cha Msingi atuambie bei anayonunulia ni shilingi ngapi na volume anayotaka kununua ni kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka transparent kwenye mfumo huu, hatulazimishi kwenda kwenye Chama Kikuu cha Ushirika. Tunamruhusu kwenda kwenye Chama cha Msingi na yoyote anayetaka aje hata jana nimekaa na wanunuzi wanaotaka kununua kwenye Vyama vya Msingi kwenye Wilaya ya Karagwe, Wilaya ya Kyerwa sasa hivi wanasaini makubaliano na Vyama vya Msingi ili waweze kununua kwa bei inayofanana na soko tusipofanya hivyo tutarudisha mifumo isiyokuwa rasmi na wakulima watanyonywa sana. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwanza nisikitike kwa kusema majibu aliyoyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri sijaridhika nayo kwa sababu yeye anasema Serikali inaelekeza wananchi walipwe baada ya siku tatu, hili jambo si sawa wananchi wamekuwa wakikaa zaidi ya miezi mtatu hawajalipwa. Kwa hiyo, mnapoleta majibu kwanza myafanyie utafiti, swali la kwanza, Je, Serikali kama msimamizi mkuu wa Ushirika ipo tayari kushirikiana pamoja na vyama vikuu vya Ushirika ili wanapokwenda kuomba hii mikopo Benki waweze kupewa haraka ili kuondoa adha ambayo wanaipata wananchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Serikali baada ya kuruhusu wanunuzi binafsi je, ni utaratibu upi ambao imeuweka ili huyu mnunuzi binafsi kahawa yake aipate ikiwa salama lakini pia huyu mkulima apate fedha yake kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Bilakwate kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu mikopo ambayo tumekuwa tukisaidia katika vyama vya Ushirika ambavyo vimesaidiwa na Serikali kwa kipindi cha miaka miwili, mitatu mfululizo ni vyama vya KDCU ambapo Mheshimiwa Mbunge anatoka, Serikali ilikichukua chama hiki kikiwa kina deni la zaidi ya bilioni saba Serikali ika-develop a bailout system na kukifanya chama hiki sasa hakidaiwi hata shilingi moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mikopo tunawasaidia na ni vyama vya KCU na KDCU tumewasaidia kupitia Tanzania Agricultural development Bank na msimu uliopita wamepata jumla ya bilioni 23 kwa ajili ya ku- aggregate kahawa kutoka kwa wakulima na wamepata kwa interest ya asilimia 9. Ndio vyama pekee ambavyo katika ukanda ule, pamoja na matatizo ya korona wakulima wa Kagera walipata bei bora zaidi ya kahawa yenye maganda kuliko kahawa ya wakulima wa nchi ambazo zimekuwa jirani na sisi. Wakati wenzetu wakipata wastani wa Shilingi 700 hadi 800 kahawa ya Kagera ilinunuliwa kwa shilingi 1,200 kwa usimamizi wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu na nitumie Bunge hili kuwaambiwa Waheshimiwa Wabunge wa Kagera wiki iliyopita tumekaa na vyama vikuu vya Ushirika vya KDCU, KCU na makampuni binafsi. Mpaka sasa ni makampuni saba yameonyesha interest ya kununua kahawa katika vyama vya Msingi, na ninarudia hatutowaruhusu kwenda kwa mkulima mmoja mmoja wataenda kwenye vyama vya msingi na sasa mikataba itakuwa tripartite itasainiwa na Chama cha Msingi, itasainiwa na Mkulima, itasainiwa na Chama Kikuu lakini chini ya usimamizi wa Bodi ya Kahawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu mnunuzi anataja bei anayonunulia na kiwango anachohitaji na atakapochukua kahawa kutoka kwenye chama cha Msingi nilazima alipe ndani ya muda usiozidi masaa 72 hayo ndio maelekezo ya Serikali.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mradi huu ni mpya kabisa katika Ukanda wetu wa Pwani ya Bagamoyo na Kata za Yombo, Magomeni, Nia Njema, Makurunge pamoja Fukayosi, wamejiandaa kuupokea mradi huu kwa ajili ya kilimo cha miwa. Sasa, je, ni lini Serikali itawapa mafunzo hawa watu, ili waweze kuzalisha kilicho bora kwa ajili ya kupeleka kiwandani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali namba mbili; katika jibula msingi Serikali imetenga hekta 3,600 kwa ajili ya outgrowers. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza akanionesha hizo hekta kusudi nisikae katika mikutano ya watu nikawaambia kwamba tumetengewa hekta 3,600 wakati mimi mwenyewe Mbunge sijazijua bado? Yuko tayari kwenda kunionesha ili nikienda katika mikutano niwaambie wananchi wangu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu maswali ya nyongeza mawili ya Mheshimiwa Muharami, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mafunzo yataanza hivi karibuni ambayo tutashirikiana na mwekezaji katika wakulima wote watakaoingia katika hiyo scheme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuwa niko tayari kwenda, baada ya Bunge hili tutakwenda pamoja tutafanya ziara na tutaelekezana wapi hiyo scheme ya outgrowing itafanyika.
MHE. STELLA S. FIAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kutokana na changamoto kubwa ya upungufu wa mafuta iliyopo katika nchi yetu, nataka kujua Serikali imejipanga vipi kuhakikisha inaleta mbegu bora ya alizeti kwa bei ndogo na ya chini ambayo kila mkulima ataweza kuimudu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kutokana na changamoto kubwa ya upatikanaji wa mbegu ya mahindi na mbolea katika Mkoa wa Songwe, je, Serikali iko tayari kuwaruhusu wananchi wa Mkoa wa Songwe kununua mbegu ya mahindi na mbolea katika Nchi jirani ya Zambia pasipo kuwabughudhi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Stella, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba wananchi wamekuwa wakinunua mbegu hasa waliopo mipakani katika maeneo ya Mkoa wa Rukwa na Mkoa wa Songwe kupitia mbegu zinazoingia kwa njia ambazo si halali. Vilevile tunajiridhisha na naweza nikamtolea mfano Mheshimiwa Hasunga akiwa mkulima katika Mkoa wa Rukwa aliwahi kununua mbegu za njia hizo na matokeo yake mahindi hayakuweza kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niahidi tu mbele ya Bunge lako kwamba hii changamoto tunaifanyia kazi na tutakaa na wadau wa maeneo hayo ili tutathmini njia nzuri ya kuingiza mbegu kihalali ambazo tuna upungufu nazo na kwa gharama nafuu kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la alizeti ni kweli kama nchi tuna upungufu wa karibu metric tons laki nne za mafuta ya kula. Hatua ambayo tunachukua mwaka huu, jana Waheshimiwa Wabunge wametupitishia bajeti, tumekaa na sekta binafsi na taasisi yetu ya ASA; mahitaji yetu ya mbegu ni kati ya metric tons 5,000 – 6,000 ambazo tutaenda kutumia kuzalisha kwenye eneo la hekari milioni 1.3 ambalo hili litatupatia zaidi ya tani milioni 1.2 za mbegu kwa ajili ya kwenda viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua tunayoichukua uzalishaji wa ndani utazalisha tani 2,000, tunakaa na ASA na waagizaji kutoka nje tutaagiza deficit ya mbegu kwa mwaka huu na tutaipeleka kwa wakulima at subsidized rate kwa sababu tumetenga fedha katika bajeti ili kupunguza bei ya hybrid kutoka Sh.30,000 kwa kilo moja angalau ifike kati ya Sh.7,000 hadi Sh.10,000 na Wizara ita-subsidize mbegu hizo ili wakulima waweze kupata kwa bei rahisi. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na upatikanaji wa mbegu ya alizeti kwa wananchi wa Mkoa wa Singida naomba nimuulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mkoa wa Singida wamekuwa wakilima kwa utaratibu wa kawaida kabisa ule ambao wanalima wakimaliza wanaweka mbegu baada ya kuuza wanabakiza kidogo kwa ajili ya kwenda kulima tena mwakani ndio utaratibu wanaoutumia mpaka sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Naibu Waziri sasa yupo tayari kwa ajili ya kwenda kukutana na wakulima wa alizeti wa Mkoa wa Singida hususan jimbo la Singida Magharibi kwenye kata za Mwaru, Mgungia, Muhintiri, Minyukhe kwa ajili ya kwenda kuzungumza nao sasa kuona namna gani ambavyo ku-in cooperate mawazo yao na ya Wizara kwa ajili ya kuhakikisha kwamba upatikanaji wa mbegu ya alizeti, zinapatikana zenye tija ili walime kilimo ambacho sio cha desturi? Ahsante sana.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hanje kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwenda ku-visit tupo tayari na tutafanya hivyo na Mwenyezi Mungu akijaalia mwezi huu wa Juni tutakuwa na Mkutano mkubwa utakaoongozwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu katika Mkoa wa Sindiga kwa ajili ya suala la zao la alizeti na kukutana na wazalishaji na wakulima wa alizeti. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, naomba commitment ya Serikali au itusaidie Serikali kuona namna iliyobora hasa kwa mbegu ambayo inaitwa Hysun inauzwa shilingi 35,000 kwa kilo mbili.

Je, Serikali sasa ipo tayari kuingiza ruzuku kwa mbegu hii ili uzalishaji wa mafuta uwe bora zaidi katika Mkoa wa Singida na mikoa mingine ambayo inalima alizeti?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba gharama ya mbegu za highbred za alizeti ni kubwa sana na sio rahisi mkulima wa kawaida kuweza kuzinunua. Kwa hiyo, mpango wa Wizara ya Kilimo kwa mwaka ujao wa fedha baada ya kupitishiwa bajeti yetu hapa ni kwamba tukimaliza mkutano wa kukutana Singida na wazalishaji wote wa viwanda vya kulizisha mafuta mpango wetu ni kutengeneza subsidy, ruzuku ili bei ya mbegu hizo kwa utaratibu tutakaoweka kwa wasambazaji ili wakulima bei yao iweze kupungua.

Kwa hiyo huo ni sehemu mpango wetu na tunaamini tutautumia katika mwaka ujao wa fedha ili kuweza kupunguza bei ya mbegu za alizeti.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikifuatilia suala hili kwa muda mrefu sana na majibu yamekuwa ni hivihivi. Naomba Serikali itoe commitment ni lini watalipa deni hili.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na kutokuwa na umakini hasa hasa katika ulipaji wa madeni ya ndani, Serikali haioni sasa ni muda wa kulipa riba katika madeni haya ya ndani pia kama vile wanavyolipa madeni ya nje na riba.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mchungahela maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la riba, mikataba ilikuwa haionyeshi kwamba kutakuwa na riba pale ambapo kunapokuwa kuna ucheleweshaji lakini siwezi kutoa commitment ya hilo jambo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu lini watalipwa nataka nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na kweli amekuwa akifuatilia yeye na Wabunge wa Mkoa wa Lindi na Mtwara na baadhi ya maeneo mengine ya nchi yetu kuhusu hawa waliogawa miche. Niwahakikishie kwamba mwaka ujao wa fedha watalipwa watu wote waliosambaza miche na sisi Wizara ya Kilimo tumeshamaliza zoezi hili na tumepeleka hazina.

Mheshimiwa Spka, vilevile waliokuwa watumishi wa umma kwa maana ya Wakurugenzi na Madiwani kwa kuwa kulikuwa na mikataba halali, haki zao zitalipwa na haziwezi kudhulumiwa kwa kuwa tu ni mtumishi wa umma. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kama ilivyo madeni kwa wakulima waliozalisha miche ambao hawajalipwa lakini Serikali inakiri kuwatambua. Pia kuna watu waliotoa huduma mbalimbali kwenye msimu ule wa korosho ambao Serikali ilinunua; watu walisambaza magunia, vifungashio na wengine sulphur. Tunataka pia Serikali itoe commitment kwa sababu watu hao walikopa kwenye mabenki, ni lini nao mtamalizana nao kwa kuwalipa pesa zao. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe. Ni kweli kwamba katika sekta ya korosho sio tu madeni yaliyotokana na msimu ambao Serikali ilinunua korosho a wakulima. Madeni yaliyotokana na Serikali/korosho zilizochukuliwa na wakulima, Serikali imelipa sehemu kubwa na imebaki kiwango kidogo kisichozidi shilingi bilioni 2.8 ambazo zimahusisha madeni ya wasambazaji wa watoa huduma lakini sekta nzima ya korosho kuanzia vyama vya msingi, Vyama Vikuu vya Ushirika, wakulima wenyewe wanadaiwa zaidi ya bilioni 66.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali hatua tuliyoichukua ya kwanza ni kukaa na wadai wote ikiwemo mabenki na watoa huduma na tukaweka utaratibu ambao tumeanza ku-collect fedha ambazo tutaanza kulipa kwa wale wanaohakikiwa na mchakato huo umekwishaanza na utaratibu unaendelea na kwa kuwa tutakuwa na kikao tarehe 6 Lindi ambacho kitaongozwa na Waziri Mkuu, naamini kwamba yote haya tutayajadili na tutatoka na majibu na wadai wote tumewaalika katika mkutano huo.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana. Vietnam mwaka 1993 ilikuwa ni nchi maskini sana na walikuwa wanapewa msaada wa chakula. Leo Vietnam wanazalisha surplus ya mpunga tani milioni 20 na hii ilitokana na geographical diversification policy kwenye kilimo. Wame- map nchi yao na ile sera wakaiweka, haikuwa ni sera blanket moja ya nchi nzima, kila mapping ya eneo wakafanya diversification wa kujua eneo gani litumie sera ipi.

Mhesimiwa Spika, je, leo Serikali yetu ina mkakati gani wa kuhakikisha kuongeza tija ya kilimo na kuipitia upya sera ya kilimo nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali alilouliza Mheshimiwa Zungu, Mbunge wa Ilala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa muda mrefu tumekuwa kama Taifa tukifanya makosa makubwa kufikiria kwamba kilimo kila zao linaweza likalimwa kila sehemu tuka- think of extensive instead ya intensive agriculture. Kwa hiyo, mkitazama hata bajeti ya mwelekeo wa Wizara ya Kilimo tumeangalia zaidi kuhangaika namna gani tunaongeza tija. Mwelekeo wa bajeti yetu katika mwaka ujao wa fedha ume- focus katika tija badala ya kufikiria kuongeza kila zao kila sehemu.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tunaomba ofisi za mamlaka ya juu, tutazindua timu mbili ambayo mojawapo ni suala la financing na nyingine ni suala la kupitia upya Sera na mtazamo wetu wa kilimo na tunaamini kwamba baada ya hapo tutakuwa na roadmap ambayo inaonyesha kila eneo litakuwa na specialty yake kutokana na competitive age yake na huko ndipo tutakapowekeza zaidi na teknolojia za kisasa katika hayo maeneo badala ya kufikiria kila zao linaweza kulimwa kila sehemu katika nchi. Kwa hiyo, huo ni mwelekeo wa Wizara na huko ndipo tunapotaka kwenda kama nchi.
MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya swali la nyongeza. Kutokana na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri yanayowapa matumaini wafanyabiashara wa usindikaji wa mbogamboga hasa kwa Mkoa wa Tabora hususan kinamama.

Je, ni lini Serikali kushirikiana na FAO inaweza kuanza mradi huu wa kuwawezesha kina mama kuweza kufanya biashara ya Kitaifa na Kimataifa?

Mheshimiwa Spika, je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi kuwezesha mazao haya ya usindikaji wa mbogamboga ambayo wakinamama wengi wa Mkoa wa Tabora wamejikita katika biashara hiyo kuhakikisha kwamba yanakuwa yana masoko ndani ya nchi na ukizingatia unaweza ukaenda kwenye hoteli nyingi hatuna mboga za asili, tunatumia mboga ambazo ni roast na zilizoungwa ungwa zaidi. Naomba kupata jibu, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naoba kumjibu Mheshimiwa Jacqueline maswali yake ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, lini tunaanza mradi wa FAO, tunaaza mwaka wa fedha unaokuja; ni mradi wa miaka mitano, tunaanzia majaribio katika Wilaya ya Kaliua ndipo tutakapoanzia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kuwasaidia wakinamama wa Mkoa wa Tabora na Watanzania wote kuweza kuingia katika masoko. Sasa hivi tunapata project pamoja na wenzetu wa SIDO ili waweze kukidhi vigezo vya viwango vinavyoweza kuwasaidia kuingia katika masoko ndio maana mmesikia katika Mkoa wa Tabora tumesema kwamba Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Umoja wa Wanyabiashara sasa hivi pamoja na SIDO inatafutwa eneo moja ambalo litakuwa ni center ya kina mama kwa ajili ya kukaushia na hapo kuweza kufanya packaging waweze ku- meet standard za masoko. Kwa hiyo, ni hatua ambazo zinachukuliwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi sio tu kuzalisha, je tunachokizalisha kinaweza kukidhi vigezo vinavyotakiwa vya sokoni, hiyo ndio kazi tunayoifanya katika sekta ya mbogamboga na matunda.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile Mkoa wa Ruvuma umejaaliwa kuwa na mito mingi mikubwa, mito hiyo ipo pia katika eneo la Jimbo la Madaba moja katika mito mikubwa ni mto huo Ruhuhu, lakini kuna Mto Hanga.

Nini sasa mkakati wa Serikali kuhakikisha maeneo hayo yote yanayofaa kwa umwagiliaji tunakuwa na miundombinu mikubwa na rafiki itakayoboresha kilimo cha mpunga na kilimo cha umwagiliaji katika ujumla wake maeneo ya Mkoa wetu wa Ruvuma?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhagama kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali sasa hivi tunachokifanya ni kufanya review ya master plan yote ya umwagiliaji na kubadili mfumo wa Tume yetu ya Umwagiliaji ili kuweza kupata tija katika miradi yetu ya umwagiliaji na kuwa na gharama ambazo ni affordable na kuna value for money, hili ni jambo la kwanza.

La pili tunachokifanya sasa hivi tutatambua maeneo ya kimkakati ambayo Serikali itaenda kuwekeza yenyewe 100% na maeneo mengine ya umwagiliaji tuta-encourage sekta binafsi kuweza kufanya hayo maeneo na kuwekeza sekta binafsi kwa makubaliano ya long term ili kupunguza mzigo. Kwasababu siyo lazima kila sehemu ndiyo Serikali iweze kujenga yenyewe. Kwa hiyo, tunafanya jitihada za namna hiyo kuweza kuzi-cruster hii miradi ya umwagiliaji katika maeneo ambayo itawekeza sekta binafsi na maeneo ambayo Serikali itakwenda kuwekeza kwenye miradi mikubwa ambayo sekta binafsi haiwezi kuwekeza.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Serikali imeanza kuwekeza fedha za awali katika scheme za umwagiliaji kama scheme ya Ilemba, Ng’ongo, Sakalilo, Mititi na Bonde la Ilembo; ni lini Serikali itapeleka fedha kumalizia hizi scheme ambazo tayari imeanza na ipo katika mipango yake?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza priority namba moja katika bajeti ya mwaka huu tunayoanza nayo ni kukamilisha scheme ambazo tulishapeleka fedha na ambazo hazijakamilika. Kwa hiyo, scheme zote zipo karibu 1000 na kidogo ambazo zimepelekewa fedha nusu/nusu hazijakamilika. Kwa hiyo, hii ni priority ya kwanza.

Kwa hiyo, nimuhakikikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine kote ambako tulishapeleka fedha na kuanza kuzifanyia kazi, tunafanya tathmini ya mapungufu yaliyopo na ukamilishaji, kwa sababu zipo scheme ambazo tulienda kujenga mifereji wakati hatujatengeneza bwawa la kuweza kuhifadhi maji, kwa hiyo, ni wastage of resources. Kwa hiyo, tunafanya hiyo tathmini na kuitambua na tuta-communicate officially kwa Wabunge kila mmoja kuweza kufahamu scheme zake zilizoko kwenye eneo lake ni lini zitaanza kufanyiwa kazi na zipo kwa sababu tuna-resource ndogo, tutapeleka scale of preference na kuchagua zipi tunaanza nazo kuweza kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, priority ya pili ya bajeti yetu ya mwaka huu kwenye fedha tulizotenga ni kuwekeza fedha kwenye mashamba 13 ya kuzalisha mbegu ili tuondokane na tatizo la mbegu katika nchi kwa sababu tuna mashamba ya kuzalisha mbegu, lakini hatujawekea miundombinu. Serikali inakwenda shambani kuandaa mbegu wakati ambapo mkulima naye yupo shambani. Kwa hiyo, ni jambo la aibu, tumeamua kwamba resource tunaweka namba moja kwenye mbegu; namba mbili kukamilisha scheme ambazo tulipelekeka fedha kidogo kidogo. (Makofi)
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri sana yanayotia moyo ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa kilimo cha mkataba ni kilimo ambacho kinahitaji mahitaji muhimu sana na mengi ili kifanikiwe mojawapo kubwa ni mbegu bora. Je, Wizara imejipangaje kuhakikisha wananchi wa Mkoa wa Singida na hasa Mkalama wanapata mbegu bora na kwa bei rahisi?

Swali la pili, kwa kuwa viwanda vingi vya alizeti Mkoa wa Singida vinafanyakazi kwa miezi mitatu tu kwa sababu ya ukosefu wa mbegu, Wizara imejipangaje kuhakikisha kwamba tatizo hili linatatuliwa Serikali inapata mapato na inatatua tatizo kubwa la mafuta ya mboga nchini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Francis Isack kama ifuatavyo:-

Kwanza nitumie Bunge lako Tukufu kuwaalika Wabunge wa maeneo ya Singida, Dodoma na Manyara katika mkutano utakaoongozwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu siku ya tarehe 13 Juni unaohusiana na suala la alizeti na mazao ya mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua tunayoichukua ya kwanza Wizara sasa hivi inafanya tathmini ya mahitaji ya mbegu zitakazochakatwa na viwanda ili kuweza kuondoa gap ya mafuta. Hatua ya pili tuta-subsidize mbegu kupitia maviwanda badala ya mbegu ya high sun kununuliwa kwa shilingi 30,000 Serikali inafanya tathmini sasa hivi tuta-subsidize kwa kiwango kisichopungua asilimia 50 ya bei hiyo ili wakulima waweze kupata mbegu hizi kwa bei rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hatua ya tatu tunayochukua gap mahitaji yetu ya mbegu kwa ajili ya kuzalisha alizeti zitakazotosheleza viwanda vyote kwa msimu wa mwaka mzima ni metric tans 3,900 na sisi kama Serikali uwezo wetu wa uzalishaji wa ndani ni metric tans zisizozidi 700. Wizara sasa hivi inafanya mchakato wa kuagiza mbegu metric tans 3,000 ambazo zitakuwa subsidize na hizo tutazigawa kwa wakulima kwa bei rahisi ili viwanda viweze kupata alizeti ya kutosha katika msimu ujao.

Kwa hiyo, kwa misimu ya miaka miwili tutaagiza gap na msimu wa tatu kwa fedha mlizotupitishia mwaka huu katika bajeti kwa ajili ya ASA tutakuwa na uwezo wa kuzalisha mbegu zote za alizeti ndani ya nchi yetu na hatutokuwa na gap. (Makofi)
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, msimu wa zao la pamba umefunguliwa tarehe 10 Mei na mategemeo ya wakulima ni kwamba wanapokwenda kuuza zao lao waweze kulipwa fedha zao.

Je, Wizara ya Kilimo imejipanga vipi kuhakikisha kwamba inawasimamia wenye viwanda wasiende kukopa zao la wakulima?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Magoto, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tumetoa waraka kupitia Bodi ya Pamba, nunuzi yoyote anapochukua pama katika chama cha msingi ni lazima mkulima awe amelipwa ndani ya muda usiozidi saa 48 na mnunuzi yeyote atakayekwenda kinyume na hili tutamfutia leseni na kumuondoa kwenye database ya ununuzi wa pamba, hakuna kukopa pamba ya mkulima, hili ni la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili tumetoa bei dira ambayo wakulima ni lazima walipwe kiwango kisicho pungua bei hiyo, lakini wakati huo huo ushindani unaendelea, bei dira tuliosema Wizara ya Kilimo haitakiwi kupungua shilingi 1,050 bei ya chini ingawa bei inayoendelea sasa hivi ushindani umefika mpaka shilingi 1,100/1,150 na kila mnunuzi aweke pango la bei yake kwenye AMCOS ili mkulima anapopima pamba yake ajuwe bei ya siku hiyo ni shilingi ngapi na viongozi wa AMCOS wahakikishe wanamlipa bei iliyoko sokoni siku hiyo.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto ina wakulima wadogo wadogo wa njegere na zao hili linapendwa sana nchi za nje; je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea mitaji wakulima hawa hasa wakulima wa Kijiji cha Bombo, Ubiri, Jogoi, Ngare na maeneo mengine ya Wilaya ya Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shekilindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitumie Bunge lako Tukufu, pamoja na kujenga mazingira mazuri ya mabenki kuendelea kuwapatia mikopo wakulima niziombe Halmashauri za nchi yetu mnatenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya kukopesha wajasiriamali, kilimo ni biashara, wajasiriamali siyo mama ntilie tu wala siyo madereva wa bodaboda. Niziombe Halmashauri pelekeni asilimia 10 mnazotenga katika Halmashauri zenu kwenye sekta ya Kilimo return on investment is 100% na wala hakuna defaulters kwenye kilimo unless kuna risk. Tuache kukopesha wachuuzi twendeni kwenye uzalishaji. (Makofi)
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri yaliyotolewa na Serikali, lakini ninataka nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri; sasa ni lini Serikali itakuja na mkakati ulio mzuri zaidi ukiangalia kwamba maji yanayopotea katika bonde lile ni mengi sana na ile tija ya kilimo haipatikani katika lile ambalo tunaita usalama wa chakula katika nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Ridhiwani.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba utilization level ya Ruvu na mito mingine mikubwa katika nchi yetu haijafikiwa kiwango ambacho tunakitarajia na tunacho-expect, lakini hatua tulizochukua sasa hivi katika mpango wa umwagiliaji wa mwaka 2018 ambao tumeuandaa kama Wizara na hivi karibini chini ya uongozi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa maelekezo ambayo tumekaa na Wizara ya Fedha kwa ajili ya kubadilisha model za financing za umwagiliaji na sasa tunaelekea kwenye mfumo wa EPC ambayo tutafanya miradi mikubwa ya kielelezo kwa ajili ya kuchagua maeneo machache na kuweza kuyapa kipaumbele na moja ya eneo ni Mto Ruvu na Mto Ruvuma.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naitwa Michael Constantine Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini.

Naomba niulize swali la nyongeza; kwa kuwa Kibaha Vijijini kuna scheme ambayo inaendelea kujengwa lakini hijaaza uzalishaji na tatizo kubwa ni mifugo kuingia na kufanya uharibifu.

Je, Serikali itatusaidiaje kuondoa tatizo hilo kuhamisha wafugaji wale kwenda kwenye eneo la ufugaji la NARCO ili wakulima wa eneo lile walime kwa uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hili ni jambo specific na ni jambo linahusu sehemu moja, nitamuomba baada ya hapa tukae tukutane ili tukae na wenzetu wa Wizara ya Mifugo ili tuweze kulijadili na kulitatua kw apamoja. (Makofi)
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, katika maeneo ambayo ameyasema Waziri kwamba yatajengewa scheme za uhakika, sikumsikia akitaja eneo la Ruvu Tambarare ya Same na Mto Ruvu huwa unaharibu sana eneo hilo. Je, ni lini sasa Serikali itawajengea watu wale scheme ya uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la mama yangu, Mama Shally kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sijataja maeneo ya Mkoa wa Tanga, Kilimanjaro; ni moja ya maeneo ambayo ni potential, kwa hiyo nawaomba tu Waheshimiwa Wabunge waweze kutuvumilia, tumeunza huu mchakato na wenzetu wa Wizara ya Fedha na baada ya bajeti tutakuwa tuna kikao cha pamoja kwa ajili ya kuchagua maeneo yote ambayo yatakuwa ni ya miradi ya kielelezo katika umwagiliaji. Kwa hiyo, kila ambapo kuna potential na upande wa Kaskazini ni eneo muhimu sana kwetu kwa ajili ya uzalishaji. (Makofi)
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali juu ya mpango wa zao hili la chai. Ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa tatizo kubwa la wakulima wa chai sasa hivi nchini ni kutokulipwa kwa wakati na wawekezaji; na viongozi wetu wa Serikali wamekuja Mkoa wa Njombe akiwemo Waziri wetu Mkuu na alitoa maelekezo wakulima walipwe kwa wakati lakini mpaka sasa wakulima hawajalipwa hela yao ya chai. Je, ni kauli ipi ya matumaini ya Serikali juu ya wananchi kulipwa fedha zao za chai? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa wawekezaji wengi waliopo sasa hasa Mkoa wa Njombe wanaonekana kutokuwa na uwezo na wakulima wamehamasika kufufua mashamba yao mengi ya chai hivi sasa.

Je, Serikali haioni haja sasa ya kutafuta wawekezaji wengine kwa ajili ya zao la chai Mkoani Njombe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Swalle kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwa niaba ya Serikali kwamba Wabunge wa maeneo ya Mufindi, Lupembe na Mkoa wa Njombe kwa ujumla wamekuwa wakifanya jitihada kubwa sana kufanya follow-up kuonesha stability ya zao la chai. Na nipitie Bunge lako hili na kuwahakikishia Wabunge kwamba kampuni zinazosuasua ni kampuni mbili; Uniliver nalipa vizuri na hana matatizo na wakulima wote wanaomhudumia. Tumebaki na changamoto na Kampuni ya DL na mwekezaji wa Lupembe Tea Company Ltd.

Kwa hiyo, kupitia Bunge lako nataka tu niwahakikishie Wabunge kwamba tumewa-summon hawa wawekezaji wawili na tutakutana nao katika Ofisi ya Wizara ya Kilimo, Mwenyezi Mungu akitujaalia kabla ya tarehe 30. Na kwa kuwa Wabunge mtakuwepo, tutawahusisha katika kikao hicho ili tuweze kufikia solution. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu mwekezaji wa Kampuni ya Lupembe, hana option either ku-implement tulichokubaliana ama apishe menejimenti kwa sababu Chama cha Ushirika ni sehemu ya shareholders wa ile kampuni; kaongoza kwa muda mrefu hatujaona performance, tutaweka menejimenti ya muda ambayo itahusisha watu watakaotoka ndani ya Serikali na ushirika na yeye ili waweze kuendesha kile kiwanda kwa sababu kwa muda mrefu tumempa nafasi na ameshindwa kutimiza wajibu wake.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika,
asante sana kwa kunipa fursa na naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na bughudha wanazopata wafanyabiashara na wakulima wa soya wa Mikoa ya Ruvuma na Mbeya kwa sababu wanazuiliwa kuuza na kununua wanavyotaka na tunajua zao hili limepata soko huko China sasa hivi. Serikali inatoa kauli gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Profesa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, position ya Wizara ya Kilimo na Serikali ipo very clear na nitumie Bunge lako Tukufu kusema zao la soya Mkoa wa Ruvuma na mikoa yote inayolima soya halimo kwenye stakabdhi ya ghala. Ninaomba Wakurugenzi wa Halmashauri, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa wasibughudhi mnunuzi yeyote anayeenda kununua kwa mkulima zao hili. Tumelisema kwa mdomo na tumeandika, tunarudia tena, asibughudhiwe mnunuzi yeyote anayenunua zao la soya, volume ya soya aina economic viability kuingiza kwenye stakabadhi ya ghala, bado volume ni ndogo. Wizara ya Kilimo ndio ina-mandate ya kutangaza zao gani liingie kwenye stakabadhi ya ghala. Tumesema mwaka huu waliondoe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao lingine ni choroko na dengu yaliyopo katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa hayaingii katika mfumo wa ushirika kwanza, tutayaingiza wakati utakapofika na tutakapoona kwamba sasa ni muhimu kufanya namna hiyo. Tumetoa guidance kwenye price wanachotakiwa Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya ni kufuatilia guided price iliyotolewa na Wizara ya Kilimo as indicated price kwenye masoko na wasiwabughudhi wanunuzi. (Makofi)
MHE. JUSTINE L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, aHsante kwa nafasi hii.

Kwanza nashukuru sana kwamba Waziri wa Kilimo ametembelea shamba la chai pale Kilolo Jumamosi wiki iliyopita na kujionea mwenyewe lile pori ambalo nimekuwa nikilisema hapa. Na kwa kuwa Benki ya Kilimo iko tayari na ina fedha tayari kwa ajili ya kukopesha mwekezaji yeyote, sasa je, ni lini ule mchakato wa kutafuta mwekezaji utaanza tena bada ya kuwa ulisimama katika kipindi hiki cha mwaka karibu mmoja uliopita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Kilolo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Waziri wa Kilimo Profesa Mkenda amekuwepo huko wiki iliyopita akiwa pamoja na Mkurugenzi wa Tanzania Agricultural Development Bank. Baada ya muda mrefu kuhangaika kutafuta mwekezaji, position ambayo tunayo kama Wizara ya Kilimo na ambayo tutaenda kuitekeleza ni kuanzisha special purpose vehicle ambayo shareholding structure itawahusisha wakulima wadogo na Tanzania Agricultural Development Bank kwa sababu wao ndio wanaleta mtaji na wao wataleta menejimenti.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mbunge kwamba ule mpango wa kuhangaika kutafuta mwekezaji wa nje tumeachana nao, tutatumia our own resources kufufua hilo shamba na tutaweka menejimenti ambayo ita- run, kwa sababu tumefanya majaribio kwenye Vyama vya Ushirika vya KAKU, Mbogwe na Chato tumefanikiwa.

Kwa hiyo, huu ndio utakuwa mwelekeo kwenye maeneo ambayo tutaweka mitaji, tutaanzisha special purpose vehicle, halafu tutaendelea kufanya biashara na ushirika utashindana. (Makofi)
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu ilituma Wizarani mara nyingi kwamba kuna mashamba hayo aliyoyataja Mheshimiwa Naibu Waziri, kati ya mashamba 33 yanayoendelezwa kwa robo moja tu katika mashamba yale yote 33; lakini kwa kuwa shamba hili la Bendhu mmiliki wake alifariki na akamwachia mwanae ambayo yupo nchini Zimbabwe na baadaye wafanyakazi wale hawajaweza kulipwa muda wote tokea mmiliki yule aliyefariki namba moja na yule aliyeachiwa shamba hilo hajaweza kuonekana mpaka muda huu. Sasa ni lini majibu ya Serikali kwamba hili shamba la Bendhu wafanyakazi wale wote wanaweza kupata haki yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini Waziri atakubaliana nami kwenda katika Jimbo la Karatu kuona mashamba haya 33 yote, ajionee kwamba haya mashamba hayaendelezwi. Kwa mfano katika Kata ya Oldeani hata mahali pa kuzika mtu hakuna kwa sababu mashamba yale yote yapo chini ya uwekezaji na wakati huo kutoka Fireland Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro imekuwa msitu mwingine baada ya Fireland ya Hifadhi ya Mamlaka ya Ngorongoro. Je, ni lini Waziri atafuatana na mimi kwenda katika Jimbo la Karatu kujionea mashamba haya hayaendelezwi katika majibu aliyotoa kwamba anaona mashamba haya yanaendelezwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Daniel, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwenda karatu mimi na yeye tumeshakuwa na maongezi tutakwenda na tutapanga tarehe pamoja ambayo tutakwenda kutembelea, kwenda kuangalia hayo mashamba na matatizo ya wakulima wa vitunguu ambao wanakabiliana nayo. Pia kuhusu Shamba la Bendhu nimeshajibu kwenye swali la msingi Serikali sasa hivi hatuwezi kusema jambo lolote kwasababu jambo hili lipo mahakamani tunasubiri shauri hili liishe mahakamani then tunaweza kufanya intervention.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini niseme wazi kwamba ninapotamka zao la kahawa aina ya Arabic katika Mkoa wa Kilimanjaro ni zao dume, ni zao ambalo linawapatia wanaume kipato. Wakati zao hili linapauka, wanaume wote sasa wanakwenda kuwabana akina mama kwenye zao lao la migomba, kwenye zao lao la mbogamboga, maharage na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, katika swali la msingi niliomba kuelezwa ni nini makubaliano ya kibiashara kati ya Serikali na wafanyabiashara wenye estates? Kwa sababu wale ndio wenye mashamba makubwa ya kahawa yanayozunguka wakulima wadogowadogo, estates hizo zikiwemo Tchibo, Machare, Kikafu na kadhalika.

Sasa ni lini Serikali itakubaliana na wakulima hao wa ma-estate wawasaidie hawa wakulima wadogo wadogo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; sina tatizo wala shida kabisa na uzalishaji wa miche kutoka TaCRI, lakini TaCRI ni kituo kimojawapo tu kinachozalisha miche pamoja na hiyo mingine aliyosema Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, je, Naibu Waziri yuko tayari sasa kufuatana na mimi mama yake, mguu kwa mguu twende katika mashamba ya wananchi tuone ambavyo zao hilo limepauka?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mama Shally Raymond kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, suala la kufuatana na Mheshimiwa Mama Shally kwenda Mkoa wa Kilimanjaro, nimhakikishie niko tayari na tutapanga mimi na yeye kwa sababu nina wajibu kwake, ni mama yangu, kanilea miaka mitano nikiwa next kwake. Kwa hiyo, nitakwenda na nitazunguka naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuingia mikataba na estates, kwanza mikataba ni willingness kati ya mtoa huduma na anayeombwa kutoa huduma, kwa hiyo, sisi kama Serikali pale ambapo watu wako tayari kuingia mikataba na Taasisi yetu ya TaCRI kwa gharama nafuu ambayo siku ya mwisho haitaweza kumuumiza mkulima na conditions ambazo haziwezi kutuumiza, tuko tayari.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa hivi tuna programu kubwa ya kuzalisha zaidi ya miche milioni 20 ya kahawa ambayo tutaigawa katika kipindi hiki cha miaka mitano. Kwa hiyo, kwa wafanyabiashara ambao wako tayari kuingia kwa conditions ambazo ziko wazi na TaCRI, sisi wala hatuna tatizo juu ya hilo na ndiyo maana tumetaja baadhi ya taasisi ambazo tumeshaingia nazo makubaliano na baadhi ya wakulima ambao tutaingia nao makubaliano. Lakini tukienda pamoja kama tutakutana na hao wenye estates kubwa tutajadiliana namna ya kufanya.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante, lakini uzalishaji wa miche ya kahawa unafanana na uzalishaji wa miche ya mikorosho iliyopo Mkoani Mtwara. Vikundi vinavyozalisha miche ya korosho Mkoani Mtwara vinaidai Serikali tangu mwaka 2018 na hivi karibuni tulipata kauli ya Serikali kwamba hundi imeandikwa.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni je, ni lini Serikali italipa vikundi hivyo vya uzalishaji wa miche ya korosho vilivyoko Mkoani Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hokororo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, nitumie Bunge lako kuwaambia kwamba wakulima wadogo wote ambao walikuwa wanadai zaidi ya shilingi bilioni 1.8, tayari fedha hizi zimeshatoka na sasa tunafanya utaratibu ili Wizara ziweze kupelekwa Bodi ya Korosho na Bodi ya Korosho ianze kulipa wakulima. Anytime kuanzia sasa fedha hizo watakuwa wameanza kuzipata.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie tu kwamba kwa sababu utaratibu tuliokuwa tumejiwekea na ninashukuru Waziri wa Fedha hapa alisema kwamba taasisi yoyote ya Serikali itakayopokea fedha dakika za mwisho, hakutakuwa na ule utaratibu wa kuzirudisha, tunaamini kwamba kati ya wiki ijayo mpaka mwanzoni mwa mwezi Julai fedha hizi zitanza kulipwa kwa sababu tayari utaratibu wake umeshakamilika.

Mheshimiwa Spika, vilevile watumishi wa umma walioingia mikataba na Bodi ya Korosho, malipo yao na yenyewe kama Wizara sisi tumesha-compile na kuzipeleka Wizara ya Fedha ili na wao waweze kupata haki yao kwa sababu kuwa watumishi wa umma hakuwaondolei haki ya kulipwa kama ambavyo walitakiwa kulipwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kuwasiliana kwa karibu kuhakikisha kwamba mpaka Julai wakulima wote fedha zao wawe wameshazipata kwa sababu fedha hizo hata zikiingia kwetu tarehe 30 hazitarudi Hazina.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, matatizo ya zao la kahawa ya Mkoa wa Kilimanjaro yanafanana sana na matatizo ya kahawa ya Mkoa wa Kagera. Mavuno ya kahawa katika Mkoa wa Kagera huanza mwezi Aprili hadi Mei, lakini mpaka juzi Vyama vya Msingi vilikuwa havijafungua msimu wa kahawa.

Mheshimiwa Spika, na tatizo kubwa lililopo hasa Wilaya ya Muleba, wananchi wanabugudhiwa na task force ambayo imeundwa ambayo inajumuisha watu wa PCCB, Usalama wa Taifa na watu wa Kilimo. Kila anayekutana naye anatoka shambani ana gunia moja anakamatwa na kupelekwa kituo cha polisi.

Naomba kauli ya Serikali, je, ni nini kauli ya Serikali kukomesha vitendo viovu hivi ambavyo vinawabugudhi wakulima kwa kisingizo kwamba wanalangua kahawa ilhali wako kwenye Wilaya yao, wako kwenye tarafa yao na vijiji vyao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Muleba Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, niseme na nirudie tena, tumefanya vikao na viongozi wa Mkoa wa Kagera, tumefanya vikao na vyama vikuu vya ushirika vya Kagera, tumefanya vikao na wanunuzi binafsi; la kwanza, hatumzuii mkulima yeyote kupitia chama chake cha msingi kuuza mazao yake kwa mfanyabiashara katika level ya chama cha msingi. Hili ni jambo la kwanza, na tumeruhusu na tumetoa leseni. Na msimu umeshafunguliwa. Na wiki iliyopita tulikuwa na mkutano hapa Dodoma wa wadau wote wa kahawa.

Mheshimiwa Spika, la pili, tuwaombe viongozi katika ngazi za Halmashauri na Wilaya. Sekta ya kilimo haiwezi kusimamiwa kimabavu, sekta ya kilimo inasimamiwa kwa misingi ya win-win. Mkulima anayevuna mazao yake kutoka shambani kuyapeleka kwenye nyumba yake ama kuyapeleka kwenye chama chake cha msingi, naomba kupitia Bunge lako niwaombe viongozi walioko katika Halmashauri na Wilaya wasiwabughudhi.

Mheshimiwa Spika, lakini haturuhusu vilevile wafanyabiashara wanaowafuata wakulima mashambani kwenda kununua mazao chini ya bei ya soko, halafu wao kupeleka kwenye minada na Chama cha Msingi ili waweze ku-benefit na bei. Hilo hatutaruhusu na wala hatutaruhusu mfanyabiashara yeyote anayechepusha mazao kuvusha kwenye mpaka wa Tanzania na Uganda.

Mheshimiwa Spika, tunawataka na nitumie Bunge lako kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, kama mna wanunuzi kutoka Uganda ambao wana uwezo wa kutupa bei nzuri, waleteni Wizarani tutawapa leseni, watakwenda kununua katika mfumo rasmi bila kubugudhiwa na mtu yeyote.
MHE. BALOZI DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali hususan kuhusu zao la parachichi, bado mikoa ya Kusini hususan Njombe, zao la mahindi limeendelea kuwa ni changamoto. Serikali ina mpango gani wa muda mrefu wa kuondokana na hii changamoto ya zao la mahindi? Ikiwa ni bei ya mahindi pamoja na changamoto ya mbolea kwa Mkoa wa Njombe na Mikoa ya Kusini?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Balozi Dkt. Pindi Chana, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja; Serikali kupitia Wizara ya Kilimo tukishirikiana na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara tumeamua sasa hivi kubadili mfumo wa uuzaji wa mazao ya kilimo badala ya kusubiri wanunuzi kuja ndani ya mipaka ya Tanzania sasa tunawafuata katika maeneo yao. Serikali sasa hivi imeanza mchakato wa kufungua maghala katika baadhi ya nchi ikiwemo nchi ya South Sudan, tunafungua ghala letu la kwanza kwa ajili ya kuuza mazao, ghala hilo litatumika vilevile na private sector pale ambapo private sector wanataka kuuza. Vilevile tunafungua ghala la kuuza mazao ya chakula katika Jiji la Nairobi kwa ajili ya kuuza processed products kwa maana ya unga wa mahindi, mchele na mafuta ya kula ya alizeti, pia tunafungua ghala katika Jiji la Mombasa kwa ajili ya kuhudumia processors walioko katika nchi ya Kenya.

Mheshimiwa Spika, pia tumeanza juhudi ya kuangalia uwezekano wa kufungua maghala katika nchi ya Kongo, especially Kongo Mashariki ili badala ya sisi kusubiri wanunuzi kuja katika nchi yetu tunahakikisha kwamba bidhaa zinakuwepo katika masoko yao na inakuwa rahisi kuwahudumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine la muda mrefu ni uwekezaji katika tija ili kupunguza gharama za uzalishaji na cost per unit na kufanya mazao yetu kuwa competitive katika masoko yanayotuzunguka. Moja ya soko kubwa ni nchi kama Kenya ambayo ina deficit ya zaidi ya tani laki sita kwa mwaka ya mahindi ambayo tunaichukulia kama ni fursa kubwa na kipato cha mwananchi wa Kenya asilimia 50 anatumia katika chakula.

Mheshimiwa Spika, hivyo, kwetu hili ni eneo la fursa na ndiyo maana tunaamua kuwekeza katika miundombinu ambayo itatumika na Serikali lakini vilevile na sekta binafsi wanaweza kutumia kuuzia hizo outlets tunazofungua katika nchi hizo. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, hitaji la wakulima kuunganishwa na wawekezaji wa nje na ndani lililopo kule Mikoa ya Kusini linafanana kabisa na hitaji la wakulima wa zao la vanilla kutoka Wilaya za Bukoba, Misenyi, pamoja na Muleba Mkoani Kagera, ningependa kufahamu Serikali ina mpango gani wa kuunganisha wakulima wa zao la vanilla na wawekezaji wa kutoka nje na ndani ya nchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli zao la vanilla linalimwa katika Mkoa wa Kagera, vilevile ni moja kati ya zao linalokua katika Mkoa wa Kilimanjaro. Nikiri tu hapa kwamba miongoni mwa Wabunge ambao wamekuwa wakilifuatilia zao hili mmojawapo ni Mheshimiwa Neema na Mheshimiwa Saasisha Mafuwe, Mbunge wa Mwanga - Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka tu niwahakikishie tumeanza mazungumzo na local exporters wa zao hili la vanilla ili tuanze kutengeneza mfumo wa contract farming moja kwa moja na mikataba. Mheshimiwa Shigongo naye ni mmoja kati ya waathirika wa zao hili, ili tuhakikishe zao hili linakua kwenye ramani, hili ni high value commodity na Wizara tumeanza kuwekeza kwenye research and development.

Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge ni zao jipya ambalo limeanza kuchukua nafasi na tunalitazama kwa ukaribu sana na kuwaunganisha na masoko. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo nami nilikuwa nauliza kuhusu vanilla, amenijibu vizuri mno na kutambua Wilaya yetu inalima zao hili.

Serikali kwa kuwa sasa imeona zao hili ambalo lina bei nzuri sana sokoni, mwanzoni ilikuwa ni 120,000 sasa hivi limeshuka kwa sababu ya kukosa watu wa kuwaunganisha, kilo inauzwa 20,000.

Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuhakikisha inatuletea wataalam sambamba na hili ambalo ametuambia la kutafutia masoko? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Bunge lako Tukufu hili mlitupitishia ongezeko la bajeti ya Wizara ya Kilimo kwenye utafiti zaidi ya asilimia 90. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge moja ya eneo ambalo tunaenda kuwekeza sana ni kwenye utafiti na training ya Wataalam hasa wanaoshiriki katika shughuli za uzalishaji kwa maana ya Wagani.

Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba, mwaka huu tunaanza program ya training na Waziri wa kilimo wiki iliyopita amezindua training ya kwanza katika Wilaya ya Mpwapwa, Mkoa wa Dodoma na zoezi hili linaendelea nchi nzima tutakuwa tuna-train kutokana na ikolojia na mazao husika ya eneo husika ya eneo husika ili kuwafanya wataalam waweze kufanana na mazao yaliyoko eneo hilo. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ni pale ambapo Serikali imesema kwamba mwaka huu kulikuwa na kampuni nane za wazawa zimeingia mikataba na wakulima. Hadi ninaposimama hapa Bungeni mwaka huu kumekuwa na kuvunja rekodi ya kuwakopa wakulima maana yake wameuza tumbaku yao mwezi wa Tano, lakini hadi ninaposimama Bungeni hapa asilimia zaidi ya 50 ya wakulima hasa waliouza tumbaku yao kwenye kampuni hizo za wazawa hawajalipwa. Hawajalipwa kwa sababu kampuni hizo ndogo zimepata shida na changamoto katika kuuza tumbaku hiyo kwenye soko la dunia. Walikuwa wanauza kupitia Zambia, wamefungiwa huko. Walikuwa wanauza kupitia Malawi, wamefungiwa huko. Sasa je, Serikali haioni hasa kama Waziri, haioni umuhimu wa kukutana na hizo kampuni nane ili kuona namna ya kuwasaidia ili hatimaye nayo yawalipe wakulima haraka iwezekanavyo? Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, kwa mujibu wa sheria, zao la tumbaku linaendelezwa na kusimamiwa na Bodi ya Tumbaku. Tangu mwaka jana Bodi ya Tumbaku imemaliza muda wake, hadi sasa hivi inafanya kazi zake kinyume cha sheria. Hivi Serikali haioni kwamba inatakiwa iteue Bodi ya Tumbaku kesho? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, Wizara ya Kilimo imeshakutana na kampuni zote nane za Kitanzania zinazonunua tumbaku na ningeomba tu-acknowledge kazi iliyofanywa na kampuni hizi za Kitanzania katika kununua tumbaku. Tumbaku yote iliyonunuliwa mpaka msimu unakwisha ni jumla ya bilioni 86. Fedha zilizolipwa mpaka sasa ni bilioni 82, kwa hiyo, sio sahihi kwamba zaidi ya asilimia 50 kwamba wakulima hawajalipwa. Tuna-acknowledge fedha ambayo haijalipwa ya wakulima mpaka sasa imebaki shilingi bilioni nne.

Mheshimiwa Spika, la pili, kwenye eneo hili tumbaku hii iliyonunuliwa na naomba Bunge lako Tukufu lifahamu kabla ya kuleta kampuni za Kitanzania katika mfumo wa ununuzi wa tumbaku pamoja na grade zaidi ya 60 za tumbaku, kulikuwa kuna tumbaku inaitwa reject inayotupwa ambayo mkulima anaitupa shambani. Ni kampuni hizi za Kitanzania ndiyo zimeenda kuinunua mpaka tumbaku inayoitwa reject na kwa mwaka huu hakuna tumbaku iliyobaki mikononi mwa wakulima. Kunapokuwa na success story, tu-acknowledge na hili ni jambo jema. Kwa miaka mingi sekta hii imekuwa kwenye dominance ya kampuni mbili tu. Tumeingiza kampuni za Kitanzania against all efforts za international market ambazo zilituzuia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu malipo yaliyobaki na tumbaku iliyoko Malawi na Zambia, Balozi Simba aliyeko Zambia ameshafanya jitihada kwa sababu walio-block tumbaku yetu isinunuliwe Zambia ni hizi hizi kampuni kubwa zilizoko ndani ya nchi, zimetumia subsidiary companies zao kule nchi kuzuia tumbaku yetu isinunuliwe. Tatizo hili tumeli- resolve, tuko kwenye hatua za mwisho. Tumeongea na Benki ya CRDB na NMB watatoa fedha ili kampuni hizi zimalizie bilioni nne iliyobaki ambayo haijalipwa kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie Bunge lako Tukufu kusema tutaendelea ku-support kampuni za Watanzania kununua green tobacco na kui-export kwa sababu tumbaku haiwezi kugeuka kuwa chapati.

Mheshimiwa Spika, la mwisho kuhusu suala la Bodi. Bodi ya Tumbaku imemaliza muda wake, ni kweli. Sisi kama Wizara tumeshapeleka mapendekezo vetting inaendelea na tumeshaomba kwa Mheshimiwa Rais ili aweze kumteua Mwenyekiti. Iko kwenye hatua za mwisho na ni interest yetu sisi kama Wizara kuhakikisha Bodi ya Tumbaku inafanya kazi yake kwa mujibu wa sheria. Sasa hivi Bodi haipo, Mkurugenzi anafanya kazi chini ya Katibu Mkuu kwa mujibu wa sheria.

Kwa hiyo, Bodi ya Tumbaku inafanya kazi chini ya DG na anaripoti moja kwa moja kwa Katibu Mkuu. Tumeshapeleka mapendekezo na tunaendelea kufuatilia Serikalini.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nimepokea maelezo yake aliyonipa katika swali langu, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa, Serikali inafahamu kwamba, suala hili la mikopo linaathiri sana wakulima wetu. Je, Serikali haioni kwamba, sasa ni wakati wa kuwafungulia milango wakulima kuweza kuuza mazao yao wao wenyewe ikiwa ndani au nje ya nchi ili kuweza kunusuru mazao yao kuharibika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa, Serikali inawajali wakulima na inawathamini. Je, kwa nini Wizara haitengi bajeti maalum kwa ajili ya kununua mazao ya wakulima yale yanayorundikana majumbani ambayo yanakosa soko ili kuweza kuwasaidia wakulima wao kunusuru nguvu zao na maharibiko ya mazao yao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fakharia, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kufungua milango Serikali imefungua milango kwa mkulima mfanyabiashara yeyote wa mazao kuuza popote pale duniani na hatazuiliwa na mtu yeyote. Wizara ya Kilimo tunatoa vibali vya export bure kwa ajili ya kuuza mazao ndani na nje ya nchi na hakuna mfanyabiashara wala mkulima yeyote atakayezuiliwa kuuza popote anapopata soko.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kuongeza bajeti kwa ajili ya kununua mazao ya wakulima, sisi kama Wizara kama utakumbuka mpaka sasa hivi Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuongeza fedha za kununua mazao pale ambapo linapojitokeza tatizo na Serikali hununua mazao kwa sababu kubwa mbili.

Mheshimiwa Spika, moja kwa ajili ya kuhifadhi; lakini mbili kwa ajili ya ku-stimulate soko pale ambapo mazao ya wakulima yanaanguka bei. Na utakumbuka hapa Bunge lako Tukufu lilileta hoja na Wabunge waliibuka na hoja ya ku- rescue zao la mahindi na Serikali na Mheshimiwa Rais akaidhinisha matumizi ya shilingi bilioni 100 ambazo tumeenda kununulia mazao na mpaka sasa tunanunua mahindi kwa shilingi 500 kupitia taasisi yetu ya NFRA na ununuzi unaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua ya kununua mazao tutaendelea kuifanya kadri ambavyo bajeti itakuwa inaruhusu na Bunge lako Tukufu likitupitishia fedha sisi tutaenda kutekeleza field. (Makofi)
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza niishukuru sana Serikali kupitia Wizara ya Kilimo kwa kazi nzuri ambayo inafanywa kwenye sekta hii muhimu sana ya zao la chai nchini. Nasi wananchi wa Jimbo la Lupembe kwa taarifa tu ni kwamba wananchi sasa wameanza kulipwa mazao yale vizuri, Serikali pia imetupatia fedha kwa ajili ya barabara za kwenye mashamba ya chai, naipongeza sana Serikali na kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri na Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuwa, Mpango wa Serikali sasa ni kwenda mbele kuboresha hili zao la chai, Lupembe tulikuwa na mgogoro wa Kiwanda kwa muda mrefu kwa miaka 17 ambao sasa umefikia mwisho. Tumekubaliana kiwanda kirudishwe kwa wabia, kwa maana ya wakulima pamoja na Serikali. Lakini mpaka sasa mchakato wa ukaguzi wa kile kiwanda ili kiweze kukabidhiwa kwa wananchi haujafika mwisho.

Je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba ukaguzi huu unafanyika haraka na kiwanda kile kiweze kwenda kwa wananchi ambao ni wakulima wa chai? (Makofi)

Jambo la pili; ndani ya Bunge lako Tukufu pamekuwa na ahadi ya muda mrefu ya Serikali, ya kuanzisha mnada wa zao la chai Dar es Salaam ambapo kwa muda mrefu chai yetu nchini inauzwa Mombasa.

Je, ni lini mnada huu wa chai utaanzishwa nchini Tanzania ili kukuza bei ya chai ya wananchi wa Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Enosy, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana na sisi kama Wizara ya Kilimo tunamshukuru kwa dhati kabisa kama Mbunge wa eneo la Lupembe, namna alivyoshiriki katika kuhakikisha kwamba mgogoro uliodumu miaka 17 unafika hatma tunakushukuru sana kwa support uliyoitoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali baada ya huu mgoogro kuwa muda mrefu na mgogoro huu tumeanza kuhangaika nao kwa zaidi ya miaka 17. Hivi sasa tumefikia tamati na tumesaini makubaliano kupitia Solicitor General kati ya pande ambazo zilikuwa zinavutana na hivi sasa ninavyoongea, Kamati kutoka Ofisi ya TR inafanya tathmini ya kuangalia baadhi ya misitu iliyokuwa sehemu ya mgogoro huo na sasa hivi ninavyoongea wako Lupembe wakifanya kazi hiyo na wameripoti siku ya jana katika Mkoa wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili ni kufanya tathmini ya investment iliyowekwa na mwekezaji ili tuone kwamba, hatutaki siku ya mwisho kudhulumu haki ya mtu. Tunataka hii situation iondoke na tuweze kufanya tathmini kwa hiyo, tunamuomba Mheshimiwa Mbunge atupe muda. Sisi kama Wizara tumeshawasiliana na Wizara ya Fedha na Ofisi ya TR, kuhakikisha kwamba mgogoro huu tunaumaliza mapema. Ili mwakani kiwanda kile kianze kazi chini ya management mpya na yule Mwekezaji tuwe tumemalizana naye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la mnada nataka tu nimwambie kwamba dhamira na maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kwamba, mnada huu unatakiwa uanze mwaka huu Disemba.

Mheshimiwa Mwenuekiti, nataka nitoe tu taarifa katika Bunge lako Tukufu leo hii hii tumemaliza kikao cha wadau, kwa sababu wazalishaji wa chai walikuwa wanahofu namna ambavyo tunauweka huu mnada na ile rule book ambayo tunaipitisha. Tumejadiliana na kuweza kukubaliana juu ya mambo yote ambayo walikuwa na hofu nayo. Sasa tunaenda hatua ya pili mnada wa chai unahitaji kuwepo kwa kusajiliwa kwa brokers ambao watafanya hiyo kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na gharama tumekubaliana tutawasajili ma-broker kutoka nchi ya Kenya na kutoka nchi ya Sri Lanka ili mnada wetu uweze kuwa na International Picture na mwisho tutawasajili bure. Leo ndiyo tumekubaliana hivi vitu, nataka nimuombe Mheshimiwa Mbunge na wadau wa chai watupe muda tutahakikisha mnada unatokea, kuna changamoto chai yetu volume ni ndogo, tunaongea na wenzetu wa Burundi ili chai yao nayo ipite katika soko la Dar es Salaam tuko katika hatua nzuri. Tunasaini MOU na Serikali ya Rwanda kati ya Wizara ya Kilimo ya Tanzania na Wizara ya Kilimo ya Rwanda Juu ya namna ambavyo nao chai yao iweze kupita katika mnada wetu. Kwa hiyo, tuko katika hatua nzuri tumeshakuwa na rule book, tumeshamaliza structure zote tumeshaweka platform na sasa tunaanza kusajili madalali watakaoshiriki katika mnada huu na mnada huu utatokea. (Makofi)
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa Wilaya ya Hanang’ ni wakulima wakubwa sana wa kilimo cha ngano na wanalima haswa, shayiri na waliingia mkataba na TBL kwa kipindi kirefu juu ya kuwapa mbegu lakini baadae kuwauzia. Kwa hiyo, kuwa na soko la uhakika lakini pia upatikanaji wa mbegu wa uhakika. Mpaka sasa TBL imekaa kimya kwa wakulima na wakulima wamekuwa na taharuki kubwa kwa sababu, msimu umefika na TBL wamekaa kimya.

Je, ni nini kauli ya Serikali juu ya kuwaondoa hofu wakulima wa shayiri wa Wilaya ya Hanang’? Tunaomba majibu ya Serikali. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halamga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme kauli ya Serikali. TBL hana excuse yoyote kuondoa mfumo wa contract farming wa zao la shayiri. Mwaka jana walitaka ku-withdraw tulikaa nao tukasaini nao makubaliano na walinunua jumla ya tani 8,000 kutoka katika maeneo yenu na leo nimeongea na management ya TBL mimi mwenyewe baada ya kupigiwa simu na Mkuu wa Wilaya watarudi kununua. Kwa sababu, mahitaji yao yote ya incentive package waliyotaka kwa ajili ya kujenga kiwanda hapa Dodoma Serikali imewapatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie Bunge lako hili Tukufu kuwaambia TBL warudi wakasaini mikataba na wakulima wa Kanda ya Kaskazini kwa ajili ya zao la shayiri kwa sababu, kilio chao Serikali ilisikiliza na tuliwapatia incentive package walizotaka na watapata msamaha wa kodi, tofauti na mzalishaji yeyote wa kinywaji wanachozalisha atakayeagiza shayiri kutoka nje. Hatutoruhusu kuagiza shayiri kutoka nje kabla ya shayiri ya ndani ya nchi kununuliwa. Huu ndiyo msimamo wa Serikali. (Makofi)
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Changamoto ya wakulima wa Lupembe kwenye eneo la chai ni sawa na changamoto inayowakabili wakulima wa parachichi kwenye Wilaya ya Ngara. Mathalani upatikanaji wa miche bora ya parachichi, masoko pamoja na bei.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwatambua wakulima wa parachichi Ngara lakini pia na kuboresha zao la parachichi Ngara? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumjibu Mheshimiwa Ndaisaba, Mbunge wa Ngara kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza yeye ni mdau wa mazao ya horticulture na amekuwa akishirikiana na Wizara katika maeneo mbalimbali. Pili, parachichi ni moja kati ya mazao ambayo kama Wizara ya Kilimo tunayapa priority kubwa kama ni zao ambalo linaweza likabeba sekta nzima ya mbogamboga na matunda. Nataka nimuhakikishie tu kama ana special case zinazohusu Ngara aje Wizarani tukae, tuweze kutatua kama ambavyo tumekuwa tukitatua matatizo ya wakulima wa chai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miche ya parachichi sasa hivi kama Wizara kupitia TOSCI na TARI, tumeanza mpango wa kutambua wazalishaji wa miche binafsi ambao wanazalisha miche ya parachichi na kuwasajili ili kuweza kulilinda zao hili siku ya mwisho lisiweze kujikuta tunaingia kwenye matatizo kama nchi. Kwa hiyo, nataka nimuombe kama ana jambo specific aje tukae tuweze kujadiliana. (Makofi)
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kilimo cha zao la pamba msimu wake ni kipindi hiki na wakulima katika Wilaya ya Kishapu na Mkoa wa Shinyanga kwa ujumla wameshaanza kulima. Lakini Wizara ninaishukuru kwa sababu wamesaidia usambazaji wa mbegu japokuwa siyo kwa wakati. Je, ni aina gani ya mbegu inayotumika sasa hivi katika msimu huu, kwa ajili ya kilimo cha pamba, kwa maana msimu uliopita mbegu tuliyokuwa tunalima haikuwa na tija kwa maana ya uzalishaji wa kutosha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia haikuwa himilivu kwa magonjwa mbalimbali. Kwa hiyo, ninataka nipate majibu Wizara inasema ni aina gani ya mbegu ambayo sasa, ni mbegu rasmi na ndio mbegu inayotumika katika kilimo cha msimu wa mwaka 2021/2022? Pia, ni nini mpango wa kuhakikisha kwamba viuatilifu vinasambazwa kwa wakati? Kwa sababu, kumekuwepo wa ucheleweshwaji wa viuatilifu ili mradi kupambana na aina mbalimbali ya magonjwa katika zao la pamba. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Butondo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza aina ya mbegu tunayopeleka ni UK08 ambayo tumekuwa nayo kwa kipindi cha kama miaka mitatu, miaka minne sasa hivi. Changamoto iliyojitokeza mwaka jana tumeitatua kwa kuhakikisha kwamba, mbegu tunazozisambaza safari hii zimeshakuwa treated na wakati zinaenda kupandwa tayari mbegu zile zina dawa. Tatizo lililojitokeza mwaka jana ni tatizo ambalo halihusiani sana na mbegu ni tatizo ambalo lilitokana na mambo makubwa mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, mbegu zilizoenda zilikuwa hazina dawa ya kupandia ambalo tumelitatua mwaka huu. Jambo la pili ambalo lilijitokeza mwaka jana kule kwenye ukanda wa pamba kuna wale machinga, mbegu ambazo sisi tulizihakikisha zinaenda shambani zikalimwe ziliuzwa na wajanja halafu wakulima waka-replace kwa mbegu yoyote anayoipata barabarani. Kwa hiyo, tumeamua kutengeneza utaratibu upya, tume-control mfumo wa usambazaji na mbegu tumeshaziwekea dawa za awali.

Meshimiwa Mwenyekiti, kuhusu viuatilifu huu ndiyo mwaka wa kwanza tunaanza na open stock ya milioni 2.5. Kwa hiyo, wakulima watakapopanda tunawapelekea na dawa immediately ili wasiweze kupata matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa maelekezo kuhusu pamba. Tuliamua mwaka huu wakulima wanunue mbegu kwa kujinunulia lakini tumeiona changamoto. Nataka niwaambie wakulima wa pamba na wadau wa pamba, tunafanya jitihada kama Wizara kutafuta fedha ku-finance mbegu hizi ili zao la pamba tuweze kuwagawia wakulima dawa na mbegu bure kama tulivyofanya mwaka jana. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wakulima wa Mkoa wa Kagera kwa muda mrefu wamekabiliwa na changamoto ya mnyauko wa migomba na haikupatiwa ufumbuzi. Hivi sasa kumekuja mnyauko na miche ya kahawa kwa hiyo, mkahawa mkubwa unanyauka. Nataka nipate kauli ya Serikali nini mkakati wao wa kuwasaidia wakulima wa Mkoa wa Kagera na hasa Wilaya ya Kyerwa na Karagwe. Kupambana na changamoto ya kukauka kwa mikahawa yao kutokana na hiyo homa ya virusi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumjibu Mheshimiwa Anatropia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi tu ni kwamba wataalam wa TARI baada ya Wizara kupokea taarifa juu ya athari ya mnyauko wa kahawa, hivi ninavyoongea leo wana zaidi ya siku Saba wako Mkoa wa Kagera kwa ajili ya kufanya utafiti na kuweza kutafuta solution.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisingependa kutoa jibu fupi ambalo halina uhakika hapa, tusubiri wataalam warudi watatupa majibu lakini tunatafuta solution. (Makofi)
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu hayo yenye matumaini makubwa nataka kujua: Je, ni lini mtaanza ujenzi wa Skimu ya Ilembe ambayo usanifu wa kina uko hatua za mwisho, ikiwa ni pamoja na kumalizia skimu ya Ng’ongo na skimu ya Sakalilo ambazo zimetelekezwa kwa muda mrefu sana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, nataka kujua pamoja na kutambua skimu ya Mititi, Ilembo na Itela, ni lini mtaanza upembuzi yakinifu kwenye skimu hizo muhimu kwa wananchi wa Kata hizo nilizozitaja?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sangu, Mbunge wa Kwela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba skimu hizi kwa muda mrefu zimekuwa idle na hazijafanya kazi yake kwa kiwango ambacho kinatarajiwa. Matatizo mengi ya mifumo yetu ya umwagiliaji imekuwa kwamba skimu nyingi zinajengwa na zinaishia njiani ama zinajengwa mifereji bila kuwa na vyanzo vya uhakika vya maji. Kwa hiyo, hatua ya kwanza ambayo nilitaka nimwahidi kwamba skimu ambazo tumeshazifanyia usanifu, tutaanza kuzitengea fedha kuanzia bajeti ya mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, nimpe commitment; nilimwahidi tulipokuwa wote Rukwa na ninamwahidi tena mbele ya Bunge lako kwamba skimu hii ambayo usanifu wake upo kwenye hatua za mwisho, ni moja kati ya skimu za Mkoa wa Rukwa ambazo tumeshaziweka katika bajeti ya mwaka kesho. Kwa sababu, usanifu tulioufanya ni usanifu kamili kuanzia chanzo cha maji na mifereji mikuu na mifereji ya primary na secondary canals.

Mheshimiwa Spika, la kuhusu kwa ujumla, nataka niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwamba sasa hivi kama Wizara na wiki hii iliyopita Waziri wa Kilimo alituagiza tukae na Tume ya Umwagiliaji. Tumeanza utaratibu mpya kabisa kwenye mifumo ya umwagiliaji kwamba hatujengi skimu nusu nusu, ni heri tujenge skimu moja katika Mkoa kwa ukamilifu, badala ya kupeleka hapa shilingi milioni 50 pale shilingi 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, watusubiri tunavyoleta katika bajeti yetu itakayokuja, tutahakikisha Ofisi za Mikoa za Umwagiliaji zinapewa uwezo. Vile vile tutakwenda kufungua Ofisi za Umwagiliaji katika kila Wilaya ili ziweze kusimamia skimu na kuzitambua skimu zote ambazo zipo katika Wilaya zetu. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa yanayomkuta Mheshimiwa Sangu huko Kwela yanafanana kabisa na yanayotokea huko Jimboni Buchosa; na kwa kuwa kilimo sasa kimeshathibitika kwamba ni uti wa mgongo na unategemewa na Taifa letu: -

Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kutembelea skimu ya Uchiri iliyopo Buchosa ambayo imetelekezwa kwa muda mrefu, akiwa katika utaratibu wa kuifufua iweze kuwasaidia wananchi wa Buchosa na Taifa kwa ujumla? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niko tayari kwenda kutembelea Jimbo la Buchosa na niko tayari kwenda kutembelea Jimbo la Sengerema kuangalia mabwawa, ambayo fedha zake zilitolewa na hayajafanya kazi vizuri. Kwa hiyo, tutashirikiana Waheshimiwa Wabunge, tutakwenda pamoja. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika skimu ya Mng’aro ambayo Mheshimiwa Waziri mara kadhaa hapa alikuwa anaitolea maelezo; na nimeiuliza lakini bado mpaka sasa fedha zile ambazo mmezitenga shilingi milioni 30 hazijafika kuboresha banio na sasa tunaelekea kuanza kwa msimu wa kilimo: -

Je, ni nini commitment ya Serikali katika jambo hili?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shangazi. Kwanza nimpongeze sana yeye binafsi pamoja na Diwani wake Ndugu Jambia Juma Shehoza kwa kuifuatilia Skimu ya Mnga’ro.

Nataka tu nimwambie kwamba tumeshatangaza tender na tarehe 18 Novemba, 2021 tender hiyo inafunguliwa ili kupatikana Mkandarasi wa kuweza kwenda kuifanya kazi na kurekebisha tatizo la skimu hiyo. (Makofi)
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru leo kwa kuniona pamoja na ufupi wangu. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya, leo umesimama. (Makofi/Kicheko)

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa ninayoiona katika utengenezaji wa hizi skimu ni ukosefu wa wataalam. Kwa mfano, nimeshtuka sana kujua kwamba Skimu ya Sakalilo mpaka leo eti haijakamilika. Yaani toka kipindi hicho mimi nikiwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, wataalam walikuwa wanatoka Mbeya miaka ya 2013 mpaka leo haijakamilika. Kuna tatizo kubwa sana katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, naomba nifahamishwe, Wizara imejipanga vipi kupata wataalam wa kutosha ili kusaidia hizo skimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Manyanya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatua ya kwanza tuliyofanya kama Wizara, kama alivyosema kwamba wataalam walikuwa wanatoka Mbeya. Sasa hivi tumevunja ofisi za kanda na sasa kila Mkoa una Ofisi ya Tume ya Umwagiliaji na tumepeleka manpower, kwa maana ya ma-engineer na kila Mkoa sasa una engineer wa umwagiliaji. Hivi karibuni tumewaruhusu ma-engineer wetu wa Tume ya Umwagiliaji, kuajiri intense ambao ni graduates kutoka University ambao ni ma-engineer wa irrigation waweze kwenda ku-beef up Ofisi za Mikoa.

Mheshimiwa Spika, hatua ya pili ambayo tunajipanga nayo ni kuhakikisha katika kila Wilaya tunakuwa na engineer wa umwagiliaji tukishirikiana na waliopo katika TAMISEMI ili tuweze kuhakikisha kwamba shughuli za umwagiliaji zinasimamiwa. Kwa mwaka ujao wa fedha tutakuwa na ofisi katika kila Halmashauri inayosimamia suala la umwagiliaji ili kuwe kuna efficiency katika kufuatilia miradi ya umwagiliaji na ku-plan ili siku ya mwisho tusifanye kazi hizi nusu nusu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na miradi mingi ya umwagiliaji ambayo iko chini ya kiwango ambacho kinachotarajiwa na hili ni suala la planning na resource. Nasi kama Wizara tumepeleka mapendekezo yetu Hazina. Tunaamini mwaka ujao wa fedha na Waziri wa Fedha alisema ndani ya Bunge lako wakati anahitimisha kwamba umwagiliaji utakuwa ni sehemu ya kipaumbel. Tunaamini itakuwa hivyo na Bunge lako litatupatia rasilimali.

Mheshimiwa Spika, hatuna tatizo la wataalamu, tuna tatizo la rasilimali fedha ambayo tumeshapeleka kwa wenzetu wa Wizara ya Fedha ili tuweze kutatua hili tatizo. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Serikali iliahidi kufanya mapitio ya usanifu wa ujenzi wa bwawa la umwagiliaji kwenye eneo la Mto Mkomazi kule Korogwe, lakini mpaka leo ahadi hiyo bado haijatekelezwa: -

Napenda kujua, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ikiwa ni maandalizi ya ujenzi wa bwawa hilo, kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji kwa watu wa Korogwe?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mnzava. Tulifanya ziara akiwepo Mheshimiwa Waziri Mkuu katika Jimbo lake na tuliahidi kupeleka wataalamu.

Nataka tu nimwambie kwamba Wizara ya Kilimo imepatiwa fedha kwa ajili ya Tume ya Umwagiliaji, OC tumeshapokea. Sasa moja ya eneo ambalo wataalam wetu na wasanifu wanakwenda kulifanyia kazi ni eneo hilo. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie tu kwamba kabla ya mwaka huu wa fedha kwisha usanifu wa bwawa hilo utakuwa umekamilika na tutaliingiza katika plan. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Changamoto ya skimu zilizopo Jimbo la Kwela kama ulivyomsikia Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya akiwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa; Serikali iliwekeza fedha nyingi kwenye miradi miwili; skimu ya Lwafi pamoja na Katongoro lakini yote haifanyi kazi: -

Mheshimiwa Spika, napenda kupata kauli ya Serikali; Serikali iliwekeza zile fedha zipotee au iliwekeza ili ziwasaidie Watanzania wa Wilaya ya Nkasi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Aida Khenani Mbunge, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali haijawekeza fedha zile ili zipotee na mapungufu yeye mwenyewe anafahamu, nilikuwa Jimboni kwake na tumeongea kwa kina kuhusu hizi scheme zilizoko katika Jimbo lake, sasa hivi kama Wizara tunafanya hatua za mwisho kupeleka fedha tuliyokuahidi ya Shilingi Milioni 100 ili fedha hizo ziweze kwenda.

Nataka tu nimuahidi kwamba mapungufu yaliyopo katika scheme zilizoko Mkoa wa Rukwa na sehemu nyingi ya nchi ni kwamba nyingi zimejengwa half way, kwa hiyo sasa hivi tunachokifanya ni kuzifanyia tathmini ili tuweze kuzirekebisha ziwe zinachanzo cha maji cha uhakika na mifereji, scheme nyingi zimejengwa mifereji badala ya kuwa na water reserve, kwa hiyo nataka nimuombe yeye pamoja na Waheshimiwa Wabunge, mtupe nafasi ili tuweze ku-rectify haya matatizo yaliyopo. (Makofi)
MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali kuanzisha block farming kwenye maeneo aliyoyataja kama kwetu Kigoma, maeneo yanayotengwa yanauzwa kwa watu kwamba hekari Tano njoo utoe pesa, lakini mojawapo ya lengo la block farming ni kuwagawia wale wananchi ambao ndio walikuwa wazalishaji wakubwa kwamba Serikali muwabebe halafu mkiwabeba kwa gharama za Serikali ile pesa mliowekeza wananchi watairudisha unapouza.

Kwa nini Serikali sasa msijiandae mkafungua maeneo makubwa mukawatoa Watanzania kwenye nusu heka kwa kaya mkawapeleka heka tano na mkavumilia tunapouza kwa sababu haya mazao ya kimkakati, tutakapouza tukaweza kurudisha hizo pesa kwenye Mfuko wa Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwijage kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, dhana ya block farming kama alivyoieleza ina njia mbili, aidha Halmashauri ikitenga eneo watu wenye uwezo waweze kununua kuwekeza na kumilikishwa eneo hilo, lakini njia nyingine ni eneo ambalo ardhi inakuwa ni mali ya Halmashauri halafu Wawekezaji wanakuja kuwekeza kwa kupewa long term leasing ambayo wao wanawekeza.

Kwa hiyo, nilitaka nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote kwamba kama Wizara tuko tayari kukutana na Halmashauri yoyote ambayo itakuwa tayari kujadiliana na sisi tutengeneze module ambayo ita attract watu wengi kuweza kuwekeza katika eneo hilo na hilo ni wazo ambalo tunalipokea na tuko tayari kuweza kujadiliana kuweza kufanikisha jambo hilo.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali wa kupunguza uhaba wa mafuta nchini pamoja na zao la mchikichi lakini Serikali ilitangaza zao la alizeti kuwa ni zao pia litakaloingia kwa ajili ya kwenda kupunguza uhaba wa mafuta ya kula nchini. Katika mkakati huo wa Serikali Waziri Mkuu alitangaza Mikoa mitatu Mkoa wa Dodoma, Singida pamoja na Simiyu kuwa ndiyo Mikoa itakuwa kinara cha uzalishaji wa zao la alizeti.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo kwenye zao hili ni upatikanaji wa mbegu bora pamoja na gharama nafuu, sasa nilitaka kujua Serikali ama Wizara wamejipangaje kwenye suala zima la upatikani wa mbegu bora ambayo pia itakuwa ni bei nafuu itakayoweza kukidhi wakulima wetu kuweza kupata mbegu hiyo?

Mheshimiwa Spika, naomba kupata majibu ya Serikali kuhusiana na zao hili la alizeti. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali tulitangaza zao la halizeti kuwa zao la kimkakati na sisi kama Wizara, ni vizuri Bunge lako Tukufu likafahamu kwamba tumetangaza Mikoa mitatu kuwa ni Mikoa kinara ikiwepo Dodoma, Singida na Simiyu. Hatua tulizochukua kwenye suala la mbegu, Wizara tumeshaandaa jumla ya tani 1,600 za standard seed ya record ambayo tunaiuza kwa shilingi 3,500. Tulichokitaka kutoka kwenye Halmashauri husika ni Halmashauri ilete mahitaji ije tuipatie mbegu, watasaini petition ya makubaliano na Wizara ya Kilimo kuonyesha kwamba hiyo subsidies rate ya shilingi 3,500 fedha yake italipwa namna gani.

Mheshimiwa Spika, tumetoa aina tatu ya namna ya kulipa, cash 50 percent ama kulipa mwisho baada ya mkulima kuvuna, tunawaomba Wakurugenzi wa Halmashauri za Dodoma, Singida na Simiyu tumeshasema tumeongea na Wakuu wa Mikoa na leo tumewaambia Wakuu wa Mikoa tulipokuwa nao kwenye kikao walete. Mheshimiwa Mbunge na wewe karibu umlete Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chemba aje tuweze kukubaliana namna ya kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu long term sisi kama nchi tunahitaji high breed seed zaidi ya tani Elfu Tano ili tuweze kuipeleka kwa wakulima. Kwa hiyo, hatua tunayoichukua kwa ajili ya mwaka ujao wa fedha ni kwamba tutaingia mikataba na wazalishaji binafsi, watu binafsi siyo lazima tuzalishe mbegu Serikali, tutasaini nao makubaliano na wapo watu ambao wameshajitokeza mfano ni mtu anaitwa Ndugu Sumri ambae ana jumla ya hekta 8,000 kule Rukwa tunaingia nae makubaliano tunampa parent seed yeye anatuzalishia sisi serikali, halafu zile mbegu ndiyo tutazi-subsidies ili wakulima waweze kuzipata, ili tuondoke kwenye vicious cycle ya mbegu ni lazima turuhusu sekta binafsi ishirikiane na Serikali na huo ndio mwelekeo wa Wizara, tunaamini baada ya mwaka mmoja ama miwili tatizo la mbegu za alizeti katika nchi litakuwa historia.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi nitoe pongezi kwa Wizara ya Kilimo kwa kufuatilia kilimo cha miwa katika Jimbo la Kilombero, na hivi karibuni Mheshimiwa Naibu Waziri alikuwa kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Serikali kuendelea kuboresha ushirika bado kuna baadhi ya watu wa ushirika ambao wanalalamikiwa na wakulima, hususan katika Jimbo la Kilombero.

Je, Waziri ama Naibu Waziri atakuwa tayari sasa kuja Kilombero ili kufanya mkutano maalum na wakulima wa miwa na kuwasikiliza kuhusu malalamiko yao kuhusiana na ushirika?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Abubakari na Wabunge wote wa ukanda wa Kilombero, Mtibwa pamoja na maeneo yote hayo, nitakuja mwenyewe binafsi, nitakuja kufanya mikutano na wakulima, nitafanya mikutano na viongozi wa Ushirika na makampuni ili tuweze kuyaondoa matatizo yaliyoko kwenye eneo hilo. (Makofi)
MHE.BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, Shirika la COASCO ambalo linashughulika na suala la ukaguzi wa Vyama vya Ushirika nchini limeonekana kuwa na upungufu wa staffs ambao kimsingi ndido wanaosimamia masuala haya ya ukaguzi. Sasa je, Serikali inasema nini kuhusiana na suala hili la kuimarisha COASCO ili suala zima la ukaguzi wa Vyama vya Ushirika ikiwemo vyama vya msingi liweze kufanyika ipasavyo?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Butondo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza tunakiri kumekuwepo na udhaifu kwenye COASCO. Hatua tuliyoamua kuchukua kama Wizara na mwelekeo wa Serikali kuanzia mwaka kesho COASCO bajeti yake ya kwenda kukagua Vyama vya Msingi na Vyama Vikuu vya Ushirika itabebwa moja kwa moja na Serikali na hawatoishi kwa kupewa fedha na Vyama vya Ushirika ambao wanakwenda kuwakagua.

Lakini la pili, sasa hivi tunafanya capacity analysis ili tuweze kufikia malengo ambayo tunatakiwa kuyafikia.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba ule utaratibu wa COASCO kwenda kukagua Chama cha Msingi ama Chama Kikuu na kuhudumiwa na chama, utaratibu huo kuanzia mwaka ujao wa fedha unakufa, bajeti yote ya ukaguzi ambayo ni ya wastani wa bilioni nne itabebwa na Wizara, nao watafanya kazi kama ambavyo tunamtengea fedha CAG.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri kutokana na suala la zao muhimu la alizeti katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo tani ambazo zimetajwa hapa tani 48 zilizosambazwa katika Mkoa wa Shinyanga na tani hizi za mbegu hazijaainishwa katika Wilaya ya Kishapu ni kiasi gani cha tani za mbegu ambazo zimesambazwa katika Wilaya ya Kishapu peke yake. Pengine katika maswali yangu ya nyongeza ni kwamba ASA ambaye ni Wakala aliyekuwa anashughulikia usambazaji wa mbegu katika Mkoa wa Shinyanga Wilaya ya Kishapu peke yake ni Wilaya ambayo ilibidi wakulima wapate huduma kutoka Kishapu kwenda Manispaa ya Mjini Shinyanga Makao Makuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; je, Serikali haioni haja ya kusogeza huduma hii ili ASA aweze kusambaza ama kutoa huduma katika Wilaya per se? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; lipo eneo katika Wilaya yetu ya Kishapu ambalo linamilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu ambayo ni zaidi ya ekari mia tatu. Je, Serikali ipo tayari kuja kuliona eneo hilo na ikiwezekana kuanzisha kilimo maalum cha zao la pamba kwa ajili ya uzalishaji wa mbegu hizi za kisasa ili tuongeze tija na upatikanaji wa karibu zaidi kwa wananchi wa Kishapu kwa ajili la suala zima la mbegu za alizeti?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Butondo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uwepo wa eneo la ekari 300 Serikali tupo tayari kushirikiana na Halmashauri husika ili tuweze kuona ni namna gani hilo eneo linaweza kutumika na kwa maslahi ya wananchi wa Kishapu, hivyo, milango ya Wizara ya Kilimo iko wazi karibu wewe na Mkurugenzi wako tuweze kujadiliana ni namna gani tunaweza kulitumia hilo eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kusogeza huduma za ASA katika Halmashauri ya Kishapu. Ninataka tu nimuombe Mheshimiwa Mbunge na niwaombe Wabunge wote, siyo rahisi kuweka ofisi ya ASA katika kila Wilaya kwa wakati mmoja, gharama za uendeshaji zitakuwa kubwa na hazina economic value. Kama Halmashauri husika ina mahitaji specific ya mbegu, tupo tayari watuletee mahitaji yao, tuya- aggregate pamoja na tuwapelee katika ngazi ya Halmashauri ama Mkoa halafu wao wenyewe waweze kusambaza katika maeneo yao na wakulima wao kama tulivyofanya katika Mkoa wa Singida na Mkoa wa Dodoma na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawa-encourage Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kishapu, mahitaji ya mbegu za alizeti za Halmashauri yake wayalete kimaandishi ili sisi tuwapelekee katika ofisi zao za Halmashauri badala ya kufungua ofisi katika eneo hilo linalohusika.
MHE. JACQUELINE N. MAONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Sasa naomba niulize swali la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, mpaka sasa hivi Serikali bado haijawa na majibu sahihi kwa wakati sahihi yanayohusiana na suala la mbolea, ambayo kimsimgi imepanda bei katika maeneo yote ya nchi yetu ya Tanzania, hususan Mkoa wa Ruvuma: Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka ruzuku kwenye mbolea ili wananchi waweze kupata mbolea kwa bei nafuu?

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, Mkoa wa Ruvuma ndiyo benki ya chakula nchini Tanzania; na bila shaka yoyote Mkoa wa Ruvuma umeongoza takribani miaka minne mfululizo kwa uzalishaji wa mazao ya nafaka: Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kiwanda cha uzalishaji wa mbolea katika nyanda za juu Kusini, hususan Mkoa wa Ruvuma ikiwa ni pamoja na kuweka benki ya kilimo katika Mkoa wa Ruvuma? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hakuna njia ya mkato kwenye sekta ya kilimo zaidi ya ku-design modal ya kutoa ruzuku. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba, ilikuwa ni vigumu kwa mwaka huu kutengeneza mfumo wa ruzuku kwenye bei ya mbolea kwa sababu, historia inaonesha mifumo ya awali iliharibu na mifumo ile ilisababisha fedha nyingi za umma kupotea na wakulima hawaku-benefit na mfumo wa ruzuku uliokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilihakikishie Bunge lako Tukufu, maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kwamba, Wizara ya Kilimo tutengeneze mechanism ambayo itatuletea mfumo sahihi wa ruzuku kwa pembejeo. Tutaleta mfumo wa stabilization fund na katika bajeti ya mwaka kesho mtaiona na tutaiwekea mkakati ili ruzuku iweze kwenda moja kwa moja kuwafaidisha wakulima. Hiyo ndiyo njia pekee itakayoweza kuwalinda wakulima wetu wadogo na huo ndiyo mwelekeo wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tungetoa ruzuku leo, tusingekuwa na framework ambayo ingeweza kumfaidisha mkulima, bali kwenda kupoteza fedha za umma na hiyo isingekuwa haki kwa nchi. Kwa hiyo, kuanzia mwaka ujao wa fedha 2022/2023 tunaleta mfumo wa Stabilization Fund itakayotumika kwenye pembejeo na pale ambapo mazao ya wakulima yanaanguka kwa sababu zilizo nje ya uwezo wetu, ili kuwalinda wakulima wetu wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kujenga kiwanda; uwekezaji wa kiwanda unaangalia variables nyingi sana, siyo tu kwa sababu eneo fulani linazalisha mazao mengi, upatikanaji wa rasilimali kwa maana ya raw materials na zipo sababu nyingine. Siwezi kutoa ahadi ndani ya Bunge lako kwamba Serikali itaenda kujenga kiwanda katika Mkoa wa Ruvuma, lakini kama atatokea mwekezaji anataka kujenga kiwanda Mkoa wa Ruvuma, sisi kama Serikali tutamsaidia na kum-support ili aweze kujenga. Tunachokifanya, tunamsaidia mwekezaji wa intracom aliyeko hapa Dodoma ili aweze kuzalisha mbolea kutokana na ikolojia ya nchi yetu na yasitokee makosa yaliyotokea huko nyuma kwenye kiwanda cha Minjingu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ambayo tunayafanya na tunawapa support. Kwa hiyo, kuna kiwanda hiki cha hapa Dodoma; na vilevile tumewasaidia Minjingu kwa ajili ya kupata fedha waweze ku-expand kiwanda chao cha Minjingu ili kiweze kufikia zaidi ya tani 100,000 tuweze kukidhi mahitaji ya nchi. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa vile uzalishaji wa chakula nchini kwa sehemu kubwa unawategemea wakulima wadogo ambao kipato chao kifedha ni kidogo kuweza kumudu kununua pembejeo za kilimo kwa maana ya mbolea na mbegu; na kwa vile kwa sehemu kubwa bei ya mbolea imeongezeka sana mwaka huu kutokana na ugonjwa wa UVIKO – 19 katika nchi ambazo zinazalisha mbolea: Ni lini sasa Serikali itahakikisha kwamba nchi yetu inajitosheleza kwenye uzalishaji wa pembejeo muhimu kama mbolea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Nini sasa mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba mbolea na mbegu zinapata ruzuku ili wakulima wadogo waweze kuzalisha kwa tija? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mhagama, Mbunge wa Madaba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la ruzuku, nataka tu nilihakikishie tena Bunge lako Tukufu kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kutengeneza legal framework ambayo itatusaidia kama Serikali kutoa ruzuku kwenye pembejeo ambazo ruzuku hizo zitakwenda ku-benefit wakulima. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu, tuko kwenye hatua za mwisho ku-design Stabilization Fund ambayo itahusika na masuala ya ruzuku na pale ambapo bei za mazao zinaanguka, Serikali inaweza kufanya intervention ili kuweza kuwalinda wakulima wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni ahadi ya Serikali na sisi tutaifanya kuanzia mwaka ujao wa fedha. Kuhusu suala la kujitosheleza pembejeo za kilimo kwa maana ya mbolea na viuatilifu, sasa hivi kama nchi sisi mahitaji yetu hayazidi tani 600,000 za mbolea. Tunacho Kiwanda cha INTRACOM ambacho kimewekeza hapa Dodoma kina capacity ya tani 600,000. Wenzetu wa Wizara ya Madini wametusaidia kutoa leseni kwa ajili ya upatikanaji wa phosphate na jana walikuwa Mkoa wa Manyara kulipa fidia wananchi waliozunguka eneo hilo. Wamelipa zaidi ya shilingi bilioni moja. Kiwanda hiki kitaanza trial mwezi wa Saba kufika mwaka kesho 2023 tutakuwa tumefika 100 percent capacity ya uzalishaji wa tani 600,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda cha Minjingu tumewasaidia wamepata financing zaidi ya Dola milioni 20 ili waweze ku-expand capacity yao wafike tani 120,000. Nataka niwahakikishie ni drive ya Serikali kuvisaidia viwanda vya ndani viweze kufanya mambo mawili; moja kuzalisha organo-chemical fertilizer na pili, kufanya blending ili tuweze ku-blend chemical fertilizer wenyewe ndani ya nchi kwa mahitaji yetu ya nchi na tuweze ku-export. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mbegu, sasa hivi tumeanza ku-review makampuni binafsi kuyaruhusu kuanza kuzalisha mbegu ili siku moja Tanzania tuache kuwa importer wa mbegu, tuanze kuweza ku-export mbegu kwenda nje kwa mahitaji yetu. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa hii nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu Mbozi wakulima wetu wamefungiwa, hawawezi kwenda kukopa kwenye Mfuko wa Pembejeo na sababu ni hao wakulima 28 ambao hawajarejesha mikopo kwenye huo Mfuko wa Pembejeo.

Je, Serikali haioni kwamba haitendi haki kuwazuia wakulima wote wa Wilaya ya Mbozi, kutokupewa nafasi ya kukopa kwenye huu mfuko kwa ajili ya hao wakulima 28? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kilimo ndiyo uti wa mgongo kwenye Taifa letu. Kwa nini basi ni ngumu kwa mkulima hasa aliyepo vijijini kukopesheka ndani ya nchi hii? Nini mkakati wa Serikali kumwekea mazingira mazuri huyu mkulima aweze kukopa kwa urahisi? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba tu kwamba baada ya Bunge aidha ni leo au kesho tuweze kukutana tujadili suala la wakulima wake wa Mbozi kama special case na tuweze kutafuta solution ya kudumu kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ambalo nataka niseme ni kweli mfumo wa fedha katika nchi yetu na mifumo ya kukopesha katika nchi yetu sio rafiki kwenye sekta ya Kilimo. Kwa hiyo, kama Wizara ya Kilimo hatua tuliyochukua sasa hivi tumeanza maongezi na wenzetu Wizara ya Fedha na vile vile kuwahusisha Banki Kuu ya Tanzania, ili tuwe na sera ya fedha ya kukopesha wakulima. Kwa sababu sera zetu za fedha na sheria zetu za mikopo zinazo guide financing kwenye uchumi na kutoa mikopo nyingi zimekaa kuitazama kama grocery ndio hivyo hivyo na sekta ya kilimo inavyotazamwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tumekubaliana na wenzetu Wizara ya Fedha ili kuja na financing na policy ya agriculture financing na SME ili iwe rafiki kuwakopesha wakulima wakati huo huo tayari tunayo instrument ya TADB, kwa sababu sasa hivi tunatumia kukopesha kutokana na case by case. Kwa hiyo, tunataka tuwe na legal frame work ili iweze kusimamia suala la ukopeshaji wa sekta ya kilimo na vile vile ukopeshaji wa value chain ya kilimo na tuwe na legal procedure ambayo inaweza kuzifanya taasisi za fedha ziweze kuifata na zisimtazame mkulima kama muuza duka wa kawaida. (Makofi)
MHE. DUSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tija ya kilimo katika mazao haya ipo chini sana kwa sababu ya mbegu duni: Nini kauli ya Serikali katika kuwasaidia wakulima hawa kupata mbegu bora ili kuweza kuongeza tija katika kilimo chao?

Pili, Serikali iko tayari kushirikiana na Mkoa wa Tanga katika kuboresha mnyororo wa thamani wa kilimo cha mazao haya?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kitandula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri, kama nchi kwa muda mrefu tulikuwa hatujayapa kipaumbele mazao haya ya viungo. Nataka tu nilihakikishie Bunge lako tukufu, kwamba kwanza tumeya-cluster kama sehemu ya mazao ya horticulture, kwa hiyo, yatasimamiwa kwa karibu na idara inayohusika na mazao haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tumekiagiza kituo chetu cha Mliongano kwamba kianze kufanya kazi ya utafiti na uzalishaji wa mbegu na miche kwa ajili ya mazao ya Hiliki na mazao ya viungo pamoja na mazao ya matunda ya machungwa ambayo yanalimwa kwa wingi katika Mkoa wa Tanga ili kuondoa matatizo yanayowakabili wakulima wetu na kuyapa center stage mazao haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kushirikiana na mkoa, nataka tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tuko tayari kama Wizara ya Kilimo kukaa nao ili tujadiliane ni namna gani tunaweza kuwasaidia wakulima hawa wadogo kwenye value chain ya mazao kama ambavyo tumeamua kuwasaidia wakulima wa mkonge kwa kuwapatia makorona; na Bodi ya Mkonge itanunua makorona matatu kwa ajili ya kuwapa wakulima wadogo wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama Wizara tuko tayari kukaa nao. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninalo swali moja la nyongeza.

Kama Serikali inaamini kuwa Ushirika ndiyo njia bora ya kufikisha huduma za kilimo kwa wakulima wadogo wadogo, ikiwemo huduma za Stakabadhi za Ghala na pembejeo hasa mbolea. Je, kwa nini Serikali katika msimu huu haikuona haja ya kutumia Vyama vya Ushirika ili kufikisha mbolea za ruzuku kwa wakulima kwa njia ambayo yenye tija zaidi?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mhagama, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, siyo kwamba tumeviacha vyama vya ushirika, sasa hivi Bodi ya Mazao Mchanganyiko ndiyo inachukuwa mbolea kwa wingi na kukabidhi Vyama vya Ushirika. Sasa hivi tumeanza utaratibu wa kutambua maghala ya Vyama vya Ushirika na Chama cha Ushirika cha Tumbaku cha Mkoa wa Ruvuma kimepewa jukumu la kuanza kupeleka maeneo ambayo sekta binafsi imeshindwa kuyapeleka.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kufanya hivyo, Mkoa wa Rukwa tutashirikiana na Chama cha Ushirika cha Mkoa wa Rukwa kwa ajili ya wakulima wa mahindi, Kanda ya Ziwa tunashirikiana na Vyama vya Ushirika vya zao la pamba kwa ajili ya kuongeza usambazaji wa mbolea ya ruzuku.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Swali la kwanza; katika Kijiji cha Mgowelo ambacho kiko katika Kata hiyo hiyo ya Nyanzwa, kumetengwa zaidi ya hekta 3000 kwa ajili ya block farming. Je, Serikali iko tayari kufanya utafiti kwenye eneo hilo na kuona umuhimu wa kuweka skimu pia kwenye hilo eneo kwa sababu ni hekta nyingi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwenye Bunge lililopita, niliomba Naibu Waziri au Waziri kutembelea eneo hili na kuangalia changamoto tunazopata za skimu mbalimbali, lakini mpaka sasa ziara hiyo haijafanyika. Je, Waziri ananiahidi lini atafika Jimboni Kilolo kwa ajili ya kutembelea na kuona tunaweza tukashauriana vipi? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, maswali yake mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kufika jimboni kwake naomba nimuahidi yeye na wananchi, nitakwenda mwenyewe baada ya Bunge hili kwa ajili ya kwenda kufanya kazi hiyo pamoja na kuangalia mwendelezo wa mradi wetu wa pamoja wa chai ambao yeye mwenyewe alikuwa muasisi wa kuanzisha huo mradi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hii block farm, naomba nimwombe baada ya kikao cha Bunge tukutane ofisini ili nimkabidhi timu ya watu ambao wataenda kufanya soil analysis na kuchukua mipaka ili tuiweke kwenye mipango ya Wizara.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Serikali ilituahidi kwamba mwezi wa Saba tungepata consultant kwa ajili ya Bwawa kubwa la Mkomazi, lakini mpaka leo kuna ukimya. Je, ni lini ahadi hii itatekelezwa?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mnzava, kuhusu Bwawa la Mkomazi yeye mwenyewe anafahamu hivi karibuni timu ya Wizara ya Kilimo ilikuwepo kule na tatizo lililokuwepo katika suala la Mkomazi, design iliyokuwa imefanyika toka awali na zile skimu zilizoko maeneo yale ilikuwa ina makosa. Kwa hiyo, wataalam wa Wizara wamefanya kazi ya kwanza kwa ajili ya kwenda kutembelea na kuangalia na nimuahidi tu yeye na wananchi wa jimbo lake, kwamba next financial year ya 2023, Bwawa la Mkomazi litakuwa kwenye miradi itakayojengwa na Wizara ya Kilimo kwa ajili ya eneo hilo na skimu zote zilizoko katika ukanda ule ambazo ziko saba.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakarabati Bwawa la Nyangokorwa lililoko Wilaya ya Bariadi ili liweze kutumika katika kilimo cha umwagiliaji?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Midimu na Wabunge wote wa Mkoa wa Simiyu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara sasa hivi inachokifanya ni kuangalia namna gani tunaweza kutumia resource ya maji inayotoka katika Ziwa Victoria na kwa kuwa kuna Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria, unayoyatoa maji Ziwa Victoria kuyaleta Mkoa wa Simiyu, sasa hivi tutashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Maji, ili tuweze ku-tap yale maji yanayotoka Ziwa Victoria ili kuweza ku-develop skimu katika Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo Simiyu, ni maeneo yenye ukame na Wilaya zote za Simiyu zina ukame na zinapata mvua za muda mfupi. Kwa hiyo, njia ya kudumu ni ya kuyatumia maji ya Ziwa Victoria kwa ajili ya kutengeneza miradi ya umwagiliaji katika Mkoa wa Simiyu.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Wizara ya Kilimo itasambaza lini mbegu za alizeti katika Halmashauri ya Mji wa Bunda?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Robert, Mbunge wa Bunda na Wabunge wote, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwaka jana tulisambaza jumla ya tani 2,000 za zao la alizeti za standard seed ambazo zilikumbana na changamoto na mwaka huu tutasambaza certified seed tani 2,500. Nitumie nafasi hii, kusema kwamba, halmashauri ambazo ziko tayari kushirikiana na Wizara ya Kilimo, zilete maombi na tukubaliane, mbegu hizo tunazozigawa kwa ruzuku ni namna gani fedha ile itarudi kwa sababu tutazigawa kwa ruzuku ya asilimia 50.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine ambao watakuwa tayari, tumeshafanya hivyo Mkoa wa Singida na maeneo mengine ambao watakuwa tayari hasa Ukanda wa Kati na Ukanda wa Kanda ya Ziwa ambako uzalishaji wa alizeti unafanya vizuri zaidi.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ninaipongeza Serikali kwa hatua hizi zinazofanya za kuwafikia wakulima, lakini hatua hizi ambazo wamezichukuwa zinalenga hasa wakulima wakubwa. Kama mnavyojua, wakulima wa Tanzania wengi wao wana uchumi mdogo, ni wakulima wadogowadogo ambao wanalima heka moja, nusu heka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni mkakati gani hasa Serikali inao wa kuwafikia wakulima wadogo ambao hawana uwezo wa kununua simu, hawana uwezo wa kununua TV au kuweza kufika kwenye warsha na maonesho ya Nanenane. Je, Serikali ina mkakati gani hasa wa kuwafikia? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu niliyoyatoa kwenye swali la msingi, Serikali inachukuwa hatua mbalimbali: Moja, sasa hivi tumeanza kusajili wakulima, kwa muda mrefu tumekuwa tukihudumia watu tusiowatambua. Kwa hiyo, sasa hivi tumeanza process ya kuwasajili wakulima kuwatambua walipo, kuchukua hadi fingerprints, vilevile tunaenda kuchukua GPS coordinate za mashamba yao, zoezi hili linaendelea.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tunalolifanya ni kumwezesha Afisa Ugani ili awe na uwezo wa kuwafika wakulima. Tunao upungufu wa Maafisa Ugani katika nchi yetu wasiozidi Elfu Saba, kwa hiyo ili kuhudumia kaya Milioni Saba inakuwa tatizo. Kwa hiyo, Serikali imewekeza kuwapatia pikipiki na sasa tunawapatia nyezo na hivi karibuni tutawapatia vishikwambi ambavyo vitakuwa vinachukua taarifa za kila mkulima aliyemtembelea katika eneo lake. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge hii extension program itatuchukua kwa kipindi cha miaka mitatu ili kuweza kufika kule ambapo tunapotaka na kutambua mkulima ni nani na kila Afisa Kilimo kukabidhiwa idadi ya wakulima atakaokuwa anawahudumia kwa siku. (Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Je, Serikali imejipangaje kuhusu masoko ya ndani na nje ya nchi ili wakulima walime wakijua kwamba masoko watapata baada ya mazao kuvunwa?

Swali la Pili, kwa kuwa hali ya hewa ya Tarafa ya Chilangala, kwa leo hii imebadilika siyo kama ile miaka ya 1970 na 1980 wakati zao hili linalimwa. Je, Serikali imejipangaje kwenda kutoa elimu kwa wakulima hawa ili waweze kulima kilimo chenye tija? Ahsante.(Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hali ya hewa na mabadiliko ya tabianchi, Wizara kupitia TARI - Naliendele na Mlingano, sasa hivi wanafanya mapping ya soil na kuweza kutoa elimu kwa wakulima kutokana na ekolojia ya maeneo husika na hili zoezi ni on going, tutakapoanza program ya soya katika Mikoa ya Kusini, TARI Naliendele moja ya jukumu lao la msingi itakuwa ni kutoa elimu kwa wakulima ili tuweze kupata tija, na ndiyo maana tunaanza eneo dogo la Wilaya ya Newala Vijijini and then baada ya hapo mwaka unaofuata wa 2023/2024 kulifanya hili zao kuwa ni zao la tatu katika Mikoa ya Kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu masoko changamoto masoko ipo hasa kwa mazao ambayo siyo ya msingi ya chakula kwa binadamu, kama mazao ya korosho na mazao mengine. Kwa hiyo, hatua ambayo tunaifanya kama Serikali sasa hivi na mtaona mwaka kesho, ni Serikali kuweka nguvu kubwa katika kuongeza thamani kwa mazao ambayo tunayazalisha ndani ya nchi na kuwasaidia private sector ambao wamewekeza katika maeneo hayo kuwapa nguvu na kuwasaidia infrastructure development ili waweze kuongeza thamani katika mazao yetu na kuhakikisha kwamba tunapata zile international certification ili tuweze kumaliza hayo matatizo.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. Mheshimiwa Waziri huu ni msimu wa kilimo kwa Mkoa wa Rukwa na Nyanda za Juu Kusini lakini mpaka sasa nazungumza, upatikanaji wa mbolea na mbegu bora Wilaya ya Nkasi na Mkoa mzima wa Rukwa una changamoto.

Ni nini mkakati wa Serikali ili msiwe kikwazo kwa wakulima hawa?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Aida, nadhani jana wakati tunafanya semina aidha hakuwepo tulitoa majibu yote ya kina kuhusu hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu eneo lake, Wilaya yake, jana nimeongea na Mkuu wa Wilaya, tumeongea namna gani baadhi ya maeneo ambayo ni Tarafa zinazo wakulima wengi ziweze kufikiwa mbolea, tumeiomba Halmashauri yake iweze kutusaidia kupata usafiri ili sisi tuweze kuwasaidia mafuta waweze kusambaza mbolea maeneo ambayo mawakala hawafiki. Lakini wakala yupo Jimboni kwako na anauza mbolea. Tatizo lililopo ni mbolea kufika vijijini jambo ambalo tunashirikiana na ofisi ya Mkurugenzi na DC kwa ajili ya kufanya hivi baada ya wewe kuleta hili lalamiko kwetu. (Makofi)
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru na ninashukuru kwa majibu yanayotia moyo ya Mheshimiwa Waziri kwa niaba ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza: -

Kwanza; kwa muda mrefu kilimo cha muhogo kimekuwa kikifanywa kienyeji na kwa vile kwa sasa soko lake ni kubwa na la uhakika ni lini Serikali itaanza kuwekeza kwenye utafiti hasa kupitia kwenye kituo chetu cha TARI Mlengano ili kuongeza tija kwenye uzalishaji wa zao hili?

Swali la pili; kutokana na uwezo mdogo wa kipato kwa wananchi wengi wa vijijini Muheza, hali inayokwamisha ushiriki wao kwenye kilimo chochote kinachohitaji muda mrefu na uwekezaji mkubwa.

Je, kwa vile nimeshasema kwamba soko la muhogo sasa hivi ni kubwa na la uhakika. Serikali haioni haja ya kuhimiza kilimo cha muhogo ambacho inachukua Miezi Tisa tu kuwa tayari ili kuongeza kipato cha wananchi hawa wa vijijini? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mwinjuma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwanza kama nchi tuna- import wanga zaidi ya tani 8,000 kwa mwaka, pamoja na tunatumia muhogo kwa ajili ya chakula vilevile tunatumia wanga kwa ajili ya viwanda hasa kwenye maeneo ya pharmaceutical, matumizi ya nguo na viwanda vya karatasi.

Mheshimiwa Spika, nataka nimwambie kuhusu varieties sasa hivi tumeshatambua variety 10 katika utafiti ambazo zina uwezo wa kutuzalishia mpaka tani 20 mpaka 40 ambazo zimegundulika na watafiti wetu wa TARI. Hatua ya pili kumpelekea mkulima variety azalishe halafu hakuna uhakika wa soko ni jambo la hatari zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumechukua hatua kama Wizara tumeshaanza vikao na viwanda vyote vinavyotumia wanga kuweza kutambua ubora wa wanga wanaoutaka ili tuweze kuwapelekea wakulima na tutengeneze mfumo wa contract farming ili yale yaliyotokea Muheza mwaka jana na mwaka juzi yasiweze kujitokeza tena.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mwelekeo wa Serikali kuhusu muhogo ni mwelekeo wa industrial pamoja na matumizi ya chakula ndani zaidi tunataka ku-push mwelekeo wa industrial na tumeanza kuchukua hatua hizo. (Makofi)
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Rungwe wakulima wa parachichi wako kwenye kilio kikubwa sana ambapo wameambiwa wanunuzi watanunua maparachichi kupitia AMCOS, AMCOS yenyewe Rungwe iko moja, masharti yamekuwa ni magumu kwamba lazima pesa wapeleke kwenye AMCOS ndio watatununulia maparachichi hao wanunuzi wa parachichi. Ni jambo la kusikitisha sana wananchi wanalia wanunuzi wote wamekimbia wameenda maeneo ya Njombe, Mbozi na maeneo mengine, pale Rungwe maparachichi yanaozea shambani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kupata kauli ya Serikali; Je, wapotayari kuwalipa fidia wananchi ambao maparachichi yao yanaozea shambani sasa hivi? Pia tupate kauli ya Serikali wanasema nini kuhusu kilimo cha parachichi?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantona Mbunge wa Rungwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa akilifuatilia hili jambo, tumeongea na Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya na tumekubaliana.

Mheshimiwa Spika, avocado siyo korosho, avocado sio pamba, avocado siyo kahawa, hauwezi kulazimisha kununua avocado kwa kukusanya kwenye Chama cha Msingi, hauwezi kulazimisha avocado kuipeleka kwenye Chama cha Msingi kwa sababu ni perishable. Kwa hiyo, tumekubaliana na Mkuu wa Mkoa waufute huo utaratibu na wameshaanza kuufuta, wawaache wakulima wenye contract na wanunuzi wauze moja kwa moja kwa wanunuzi wao. Wahakikishe tu Serikali inapata ushuru wake stahiki katika njia halali na wafute tozo zote walizoziweka ambazo hazijaidhinishwa na Wizara ya Kilimo kwenye zao la avocado. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri hilo katazo linafanywa lini, kwa sababu maparachichi yanaoza. Mkuu wa Mkoa hilo katazo atalifanya lini?

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, katazo hili nimeongea na Mkuu wa Mkoa siku Mbili zilizopita na tumeshakubaliana na Wizara ya Kilimo imemwandikia barua Mkuu wa Mkoa siku ya jana kumueleza haya ambayo ninayasema. Kwamba, avocado haiwezi kuuzwa kwenye mfumo ambao unataka kufanyika Rungwe.

SPIKA: Hilo limeshaeleweka mmempa maelekezo ya hilo katazo lini, kwa sababu haya mazao yanaharibika. Kwa hiyo, kama atakuja kutoa hilo katazo baada ya miezi mitatu hiyo ndiyo hoja. Katazo linatoka lini? (Makofi)

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, katazo limetoka juzi kwa simu jana limekwenda kwa barua. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa vile bei za miche ya kisasa ya kahawa, ya miparachichi hiyo tunayozungumza, ya migomba bei zake ni juu sana. Sijui Serikali ina mpango gani wa kutoa ruzuku kwa miche hiyo? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kimei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka ujao wa fedha tutakapopitisha bajeti hapa mtaona kwenye bajeti ya Wizara ya Kilimo inatoa guidance juu ya subsidy kwenye zao la avocado na baadhi ya mazao na mazao haya kwa muda mrefu yalikuwa hayana guidance, hayajulikani nani mzalishaji kila mtu anajizalishia barabarani.

Kwa hiyo, tunazindua guiding ya uzalishaji wa miche ya avocado na mazao ya miti na kutakuwa kama ambavyo mzalishaji wa mbegu anavyozalisha na hapo mtaona kwenye bajeti tutatenga fedha kwa ajili ya ku-subsidize uzalishaji wa miche milioni 20 kuanzia mwaka kesho kwa uwezo wa Mungu. (Makofi)
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Katika nchi yetu kati ya matatizo makubwa tuliyonayo ni tatizo la ajira hasa kwa vijana wetu na tunatambua kabisa kwamba Wizara ya Kilimo ndiyo inayoweza kupunguza tatizo hili.

Je, Mheshimiwa Waziri umejipangaje katika WIzara yako kuhakikisha kwamba kilimo kinasaidia kupunguza ajira hasa kwa vijana wetu? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Manyinyi Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sekta ya kilimo ni sekta ambayo kweli inaweza kuajiri watu wengi sana lakini yapo mambo makubwa manne ambayo kwa muda mrefu yamewafanya vijana kutokuwa tayari kwenda kwenye sekta ya kilimo:

(i) Upatikanaji wa ardhi,
(ii) Upatikanaji wa mitaji,
(iii) teknolojia, na
(iv) soko la uhakika.

Mheshimiwa Spika, hii imewafanya vijana wengi kutokwenda huko. Kwa hiyo, kama Wizara tutakapokuja kusoma bajeti mwaka huu mtaona tuna-launch kitu tunaita ‘building a better tomorrow’ na tutaitengea fedha katika bajeti.

Mheshimiwa Spika, tunaanzisha block farm system ambako Serikali itachukua maeneo makubwa itayasafisha, itapima afya ya udongo, tutagawa block farm na kuwamilikisha vijana hayo maeneo.

Mheshimiwa Spika, kama ni eneo linahitaji fidia tutalipa sisi na yale maeneo yatakuwa owned na hao vijana ambao watakuwepo hapo na kuwaunganisha moja kwa moja na soko na kuijua afya ya udongo na mazao yatakayozalishwa kwenye eneo hilo. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Zao la parachichi ukienda kwenye soko la nje inaonekana parachichi nyingi zinatoka kwenye nchi ya jirani, lakini uzalishaji mkubwa unafanyika Njombe na Mikoa ya Tanzania. (Makofi)

Ni lini tutatengeneza ownership ya soko hili la parachichi lionekane ni la Tanzania na siyo la nchi jirani ambao wanunuzi wengi wananunua Tanzania na wanafanya packaging kwa jina la nchi ya jirani? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sanga la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sababu za parachichi zetu kuwa- branded nje ni kwa sababu sisi kama nchi tumekuwa kwa muda mrefu hatuna infrastructure. Kwa hiyo, watu wanakuja kununua raw wanapeleka wanakwenda ku-brand nje.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuanzia mwaka kesho tutatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa common use facility tatu, moja tutaijenga Mkoa wa Iringa ambapo itafanya kazi ya sorting, grading na branding na yeyote anayenunua huko atanunua akifikisha pale ataikuta hiyo huduma inafanyika na itakuwa-branded kama produce of Tanzania.

Mheshimiwa Spika, vilevile, zipo kampuni ambazo sasa hivi zimeshaanza ku-brand parachichi yetu na kui-brand kama produce of Tanzania kama Eat Fresh na Kampuni zingine ambazo zipo katika Nchi yetu. Kwa hiyo, jambo hili lipo na Serikali tunachukua hatua kuanzia mwakani tutakuwa na common use facility tatu moja Dar es Salaam, moja Iringa na moja Kilimanjaro. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Spika, ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo; Je, Wizara ya Kilimo ina mpango gani wa kuhamasisha na kuimarisha uwekezaji kwenye zao la vanilla kwa Mkoa wa Kagera? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Lugangira kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama Wizara zao la vanilla halikuwa kwenye map ya Serikali na kuonekana kama ni zao ambalo lina-attract na kuweza kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, nataka tu niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge baada ya kujitokeza wanunuzi na wakulima wengi either kutapeliwa au kufanya nini, tumeanza kuchukua hatua sasa hivi na tunavyoongea sasa hivi timu yetu ya Wizara ya Kilimo iko Mkoa wa Kagera na wengine wameelekea Mkoa wa Njombe kwa ajili ya kuweza kuangalia map na kuweza kulitambua vizuri na kulitengenezea mkakati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuanzia mwaka ujao wa fedha baada ya mwaka mmoja kutakuwa na mkakati rasmi wa nchi kuhusu zao la vanilla. (Makofi)
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu kwa kuwa mashamba ya Murujanda, Sechet ambayo yako chini ya Mwekezaji kwa sasa uzalishaji uko chini ya kiwango na aliahidi kwamba ndani ya mwaka mmoja ataboresha.

Wizara ina kauli gani katika kuhakikisha kwamba tunapata Wawekezaji ambao wako makini au kuwapatia wana Hanang’ maeneo hayo?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Hanang’ kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna mashamba yalichukuliwa na Wawekezaji mojawapo ni Ngano Limited katika Mkoa wa Manyara Wilaya ya Hanang’ na uwezo wake wa kuyatumia hauzidi asilimia 30. Aliingia makubaliano nasi kama Wizara ya Kilimo na kutuambia kwamba tumpe span ya mwaka mmoja, ataweza kufanya matumizi kwa kiwango cha asilimia 100 mpaka sasa amefeli.

Mheshimiwa Spika, hivyo, Wizara sasa hivi tunawasiliana na wenzetu wa TIC na kuwasiliana na wenzetu wa Hazina ili tumuite Mwekezaji huyu, tukae naye aweze ku- offload hekari zaidi ya 30,000 ambazo ameshindwa kuzitumia mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninatumia Bunge lako Tukufu kuwaambia Halmashauri ya Hanang’ kwamba eneo la Basutu lisibadilishwe matumizi litabaki kuwa eneo la uzalishaji wa ngano. Hili ni jambo muhimu sana na Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Baraza la Madiwani, wahakikishe hawabadilishi eneo la Basutu kulipelekea matumizi mengine isipokuwa kwa ajili ya matumizi ya ngano. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na unyanyasaji sana kwa wanunuzi wa parachichi wanachagua wao kusema haya yamekuwa reject, haya yamekuwa mazima.

Serikali inasaidia nini wakulima kuonesha kama kweli yale ni reject kwa sababu, wanawaonea ili wao wakapate faida zaidi? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, labda tu niseme kitu kimoja kwamba ninamuomba Mheshimiwa Mwakagenda na nitumie nafasi hii kama kuna wanunuzi wowote wanatumia hiyo nafasi kwa ajili ya kuwadhulumu wakulima na kuzitaka Halmashauri zote kuhakikisha kwamba mnunuzi yeyote anayeingia kununua parachichi katika Mkoa au Wilaya husika afuate guiding na manual ambayo Wizara ya Kilimo imeitoa. Kama kuna special case kwenye maeneo maalum ofisi yetu iko wazi tunaomba hizo taarifa tutachukua hatua. (Makofi)
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Ni kwamba Sengerema inazo skimu Tano, katika hizi skimu Tano skimu Mbili ndiyo zimepata fedha. Sasa, nataka kupata majibu ya Serikali skimu Tatu zilizobakia; Je, lini zitapata fedha kwa ajili ya kufanya usanifu?

Swali la pili, Sengerema tunao Ushirika wetu wa Nyanza ambako kuna viwanda vitatu viko katika Wilaya ya Sengerema. Hatujawahi ku-gin pamba leo ni miaka 20.

Je, Wizara ina mpango gani kuhusiana na Ushirika katika Wilaya ya Sengerema? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumwambia Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Sengerema kwamba mwaka ujao wa fedha tunajenga skimu mbili katika Wilaya ya Sengerema. Vilevile, tutatenga fedha zaidi ya Shilingi Milioni 300 kwa ajili ya kufanya usanifu kwenye skimu zilizobaki, ambazo zitatengewa fedha mwaka unaofuatia. Kwa sababu, hatuwezi kujenga skimu zote tano, kwa wakati mmoja. Kuhusu suala la Ushirika nataka nitumie nafasi hii na ninapongeza baadhi ya Vyama vya Ushirika katika nchi yetu ambavyo vimeweza kufufua ginneries. Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza kwa mwaka huu tumekubaliana Nyanza na Tanzania Agricultural Development Bank na sasa hivi ninavyoongea TADB wanafanya survey Nyanza, wanafanya survey SIMCU, wanafanya survey SHIRECU kwa ajili ya kufufua ginnery za vyama hivi vitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona kwamba mfumo huu wa kuwa na ginnery zinazomilikiwa na Vyama vya Ushirika na Vyama vya Ushirika kuwa na kampuni zao narudia. Vyama vya Ushirika kuwa na kampuni zao ambazo zinaingia kwenda kununua pamba kuongeza ushindani inamsaidia mkulima.

Mheshimiwa Spika, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, baada ya survey ya TADB katika ginnery za Chama Kikuu cha Ushirika cha Nyanza, tutakutaarifu kwamba ni ginnery gani ya Nyanza inafufuliwa sasa hivi. (Makofi)
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa nina maswali mawili ya nyongeza.

Kutokana na ongezeko kubwa la mbolea katika msimu huo uliopita, Je, sasa hivi Serikali sikivu ya CCM inaweza sasa kwa msimu unaokuja kuweka mpango wa kutoa ruzuku ya mbolea kwa wakulima wa mazao ya chakula mahindi na mpunga kwa utaratibu mtakaoona unafaa. (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa wakulima wa mahindi msimu huu wamelima kwa gharama kubwa kutokana na bei ya juu ya mbolea. Je, Serikali inaweza kwa msimu huu wa mavuno ikatangaza bei yake mapema NFRA ili wakulima waweze kupata unafuu au bei dira katika soko la mazao ya mahidi. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Vita Kawawa ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bei elekezi ya NFRA immediately baada ya Bunge lako Tukufu kupitisha bajeti na tutakapo table bajeti ya Wizara ya Kilimo na bajeti hiyo kupitishwa na Bunge lako Tukufu NFRA itatoa bei ambayo tutanunulia mazao ya nafaka kutoka kwa wananchi. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge wasubiri hiyo itafanywa baada ya Bunge la Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hoja ya ruzuku ninataka nitumie nafasi hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, maelekezo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimwa Samia Suluhu Hassan ni kwamba mwaka ujao wa fedha baada ya Julai Mosi, tumepewa jukumu Wizara ya Kilimo na Wizara ya Fedha kukaa chini pamoja kutengeneza muundo wa namna ambavyo tutatoa ruzuku kwenye mbolea na siyo tu kwenye mazao maalum tutatoa ruzuku ya mbolea kwa mazao yote ya kilimo ili kutokurudia makosa yaliyokuwepo huko awali. (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi.

Kwa kuwa Wizara ya Kilimo iliongezea fungu Benki ya Maendeleo ya Kilimo kwa lengo la kuwasaidia wakulima wadogo wadogo, inaonaje kama itatenga percent ya fedha hizo kwa ajili ya kutumia ruzuku ili bei ya mbolea kwenye msimu unaokuja iwe sawa na vile wananchi wamezoea ili kuwaondoa kwenye changamoto na majonzi ambayo wameyapitia katika msimu uliopita kwa mfumko mkubwa wa mbolea ambao wameupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Condester kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutatumia instrument gani kwa ajili ya kutoa ruzuku. Niwaomba Waheshimiwa Wabunge wasubiri kwamba tumalizane kazi tunayoifanya kati ya Wizara ya Fedha na Wizara ya Kilimo kama tutatuma through TADB, tutatumia mfumo mwingine wowote ule tutalitaarifu Bunge lako Tukufu, uhakika tu ni kwamba kuanzia Julai tutatoa ruzuku kwa ajili ya kushusha bei ya mbolea. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Waziri pamoja na bei elekezi ambazo zimekuwa zinatangazwa kila wakati, lakini bado imekuwa haitekelezeki kutoka kwenye Mkoa mmoja kwenda Mkoa mwingine hasa Mikoa ile ambayo ni big five kwa uzalishaji wa chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa changamoto hiyo ya uzalishaji ambayo ilikumba na nchi nyingine zote lakini kuna nchi ambazo bado zilifanya vizuri. Je, upo tayari kwenda kujifunza kwenye nchi ambazo nazo zilipata hiyo changamoto ya COVID lakini bado bei ya mbolea iliendelea kuwa nzuri au yenye unafuu wa kwa wakulima ikiwemo Ethiopia, Zambia, Uganda na maeneo mengine. Mpo tayari kwenda kujifunza kwa kuwa ni jambo jema. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba wataalam wa Wizara ya Kilimo wamekwenda Rwanda kwenda kuangalia subsidy scheme ya Rwanda inafanya kazi namna gani, wengine wamekwenda Zambia kwenda kuangalia subsidy scheme ya Zambia inafanya namna gani, wengine wamekwenda Malawi wameenda kuangalia subsidy scheme ya nchi hizo inafanya namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu niwaambie Waheshimiwa Wabunge ni kwamba jambo la subsidy kwenye nchi linahitaji mambo mawili, moja political will na ninamshukuru Mheshimiwa Rais ameonesha utashi wa kisiasa kuwepo kwa subsidy lakini la pili ni management ya mfumo wa subsidy. Nchi yetu ilikuwa na mfumo wa subsidy ambayo ulikuwa abused lakini ukiutazama mfumo ule ya subsidy uliokuwepo ambao ulikuwa abused it was ni mfumo ambao abuse ilitokana na systematic system ambayo ilitengenezwa na kuanzia na aliyekuwa anausimamia mpaka aliyekwenda kuutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka niwahakikishie tu kwamba Waheshimiwa Wabunge ni kwamba tutafanya mfumo wa utoaji wa ruzuku ambao hautoweza kuturudisha kule ambako tumetokea na utashi wa kisiasa wa Mheshimiwa Rais umeonekana hadharani na tarehe Nne mbele ya Watanzania aliahidi na alitoa agizo. Kwa hiyo, mtuachia tulifanyie kazi tuta- communicate na watanzania na kuwaambia namna gani tunalifanyia kazi hili jambo. (Makofi)
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuondoka kwa kampuni ya TLTC hapa nchini kumechangia kudorora kwa soko la Tumbaku.

Je, ni lini Serikali itakamilisha mazungumzo na kampuni hii ili iweze kurudi Tanzania kununua Tumbaku za wakulima na kuongeza tija na ushindani? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu niwaambie wakulima wa Tumbaku na niwaambie Watanzania, kiwanda kilichokuwa cha TLTC na kampuni ya TLTC imenunuliwa na sasa hivi amepatikana mwekezaji mwingine na mwekezaji huyu yupo kwenye hatua za mwisho na mwaka huu kiwanda kile kitafunguliwa. Serikali tunawasaidia wawekezaji wapya kuweza kupata minimum quantity ya tumbaku ili kiwanda kile kifunguliwe, kwa hiyo nataka niwaambie tu wakulima wa tumbaku kilichokuwa kiwanda cha TLTC amerudi sokoni kupitia kampuni nyingine ambayo imeweza kununua kiwanda kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niwahakikishie tu kwamba kiwanda kile kinafunguliwa na ninaamini msimu ujao wa 2022/2023 uzalishaji na makisio yataongezeka tofauti na tulivyokuwa sasa hivi. (Makofi)
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwakuwa Benki hii ya Kilimo imeanzishwa kwa namna ya kuwasaidia wakulima wa Tanzania na hii benki inapatikana katika center ya Makao Makuu.

Je, Wizara ina mkakati gani wa hii benki hata kama itashindikana kwa kila Mkoa angalau iende kwenye kila ukanda wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo moja kwanza ieleweke Tanzania Agricultural Development Bank, siyo Commercial Bank is a Development Bank. Kisera tusitajarajie nami nataka niwe mkweli mbele ya Bunge lako Tukufu. Tusitarajie TADB kuwa na matawi kama alivyo CRDB na NMB, huo ndiyo ukweli. Jukumu la kisera la TADB ni Benki ya Maendeleo ambayo moja ya function yake ni ku- de risk sekta ya kilimo kwa kutoa dhamana kwenye commercial banks, ili commercial banks ziweze kuwakopesha wananchi, hili ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tumeitaka TADB iwe na ofisi katika Mikoa na Kanda, sasa hivi Kanda ya Kati wapo, Kanda ya Magharibi wapo, Kanda ya Ziwa wapo, Kanda ya Kaskazini wameshafungua ofisi. Kwa hiyo, wana ofisi zao. Wanachokifanya sasa hivi TADB ni kuwa na makubaliano na commercial banks ambazo zitafanya kazi na wao na wao wanatoa dhamana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie Bunge lako kuwaambia sekta ya kilimo sasa hivi imekuwa ikipata mikopo mingi sana kutokana na guarantee zinazotolewa na Tanzania Agricultural Development Bank. Tunaendelea majadiliano na TADB kuboresha na kufanya awareness kwamba namna gani huduma zao zinaweza kuwepo katika taasisi za benki, katika Mikoa na Wilaya ili angalau wawe na madawati waweze kufanya kazi vizuri na Commercial Banks.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tusidhani kwamba TADB ni kama ilivyo CRDB, NMB ama ilivyo Akiba Commercial Bank hii ni Development Bank ina majukumu yake ambayo yamewekwa wazi. Nasi tunawaomba Waheshimiwa Wabunge tuache kuitaka TADB kwenda Wilaya, bali tui- demand TADB itoe dhamana kwenye Commercial Banks ili wakulima wadogo wadogo wasiokuwa na dhamana waweze kukopesheka kirahisi na Commercial Banks. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kumuuliza Waziri swali la nyongeza kwamba kumekuwepo na malalamiko kwa wananchi kuhusu ubora wa mbolea zinazoingizwa nchini na makampuni mbalimbali hasa mahindi na mazao ya kunde.

Je, ni nini hasa kauli ya Serikali kuhusu mbegu hizo ambazo zinaingizwa na hazina ubora nchini na wananchi wanaendelea kupata hasara? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Noah kwa ufupi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Mtanzania ambaye amenunua mbegu na ana receipt ya duka lililomuuzia mbegu ile na mbegu ile ikawa ni fake, atoe taarifa Wizara ya Kilimo, kwa sababu tutamchukulia hatua muuzaji kwa maana ya dealer na distributor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo utaratibu wa kisheria ambao unasimamiwa na taasisi yetu ya TOSCI na TOSCI anatoa namba maalum katika kila mbegu inayouzwa mtaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna Mtanzania amenunua mbegu na ikawa feki tunamkaribisha afike Wizara ya Kilimo, tutachukulia hatua wote. Tunayo kesi Mkoa wa Ruvuma ambayo mtu aliuza mbegu, alizitia rangi na sasa hivi amepelekwa mahakamani, anachukuliwa hatua kwa sababu huu ni uhujumu uchumi na hatuwezi kuruhusu hili. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kumekuwa na uonevu mkubwa sana na wizi mkubwa wa wananchi wanapoenda kuuza mazao yao sokoni, kuna watu wanaitwa madalali hawa watu ndio wanao panga bei ya mazao na kuondoa fursa ya wakulima kupanga bei ya mazao yao. Je, Serikali ina mpango gani wa kisheria wa kuondoa tatizo hili na kuweza kumlinda mkulima aweze kuuza kwa bei anayotaka yeye?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kumekuwa na changamoto ya uuzaji wa mazao kwa kulazimishwa kuuza kwa rumbesa wakulima wetu. Je, Serikali ni lini itapeleka maagizo maalum kwenye halmashauri zetu za kuzuia uuzaji huu wa rumbesa mazao ya wananchi?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Saashisha, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la rumbesa kama alivyojibu Naibu Waziri wa Viwanda hapa mbele ya Bunge lako tukufu vilevile Wizara ya Kilimo tukishirikiana na Wizara ya Viwanda tumeshakuwa na mwongozo rasmi ambao tutaupeleka katika halmashauri zote nchini ili halmashauri waweze kusimamia mwongozo huo kuanzia suala la ununuzi, suala la uwekaji kwenye vifungashio na namna ambavyo mazao yanasafirishwa kwa hiyo hili ni jambo ambalo tutashirikiana pamoja na Serikali za Mitaa kuhakikisha tunalitatua hili tatizo ni kweli lipo na ni tatizo kubwa lakini naamini litakwisha.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hili la madalali walioko masokoni. Kwanza uwepo wa middle man katika biashara ni jamba ambalo limekuwepo toka historia ya Dunia inaumbwa na ni jambo ambalo halikwepeki lakini kuwa na watu wakati ambao hawako regulated hili ndio tatizo ambalo linatukabili kwa hiyo Serikali kupitia Sheria iliyoianzisha Mamlaka ya COPRA hivi karibuni tumeshapeleka mapendekezo atateuliwa Mkurugenzi Mkuu wa COPRA ambaye atakuwa na jukumu la kudhibiti wauzaji na wanunuzi wanaosimamia uuzaji na ununuzi wa mazao katika masoko makuu na masoko ya awali. Kwa hiyo tutaweka utaratibu wa wazi wa kikanuni kwa kufuatana na Sheria ya COPRA ili kuweza kudhibiti na kuhakikisha kwamba mkulima anafaidika na jasho lake.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa kumekuwa na changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa mbegu za shayiri. Je, Serikali haioni sasa haja ya kuanzisha kituo cha uzalishaji wa mbegu katika shamba la NAFCO lililoko Wilaya ya Hanang?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba tu kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba shamba la Bassotu kama Wizara, tunaligeuza kuwa ni center of excellence kwa ajili ya kuzalisha ngano na shairi.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini Serikali ilituhakikishia kwamba kwa msimu wa 2022/2023 pembejeo zitafika kwa wakati kwa sababu upuliziaji baadhi ya maeneo huanza mwezi Mei. Kwa takwimu ambazo Mheshimiwa Waziri amezitoa, ukiangalia sulphur imefika tani 1,600, bado tani 23,400 lakini viuatilifu vya maji hadi sasa vimefika lita 730,724 bado lita 770,000. Je, Serikali imejipangaje ili kutokurudi kule ambako mwaka jana tulipata changamoto sana ya upatikanaji wa mapema wa pembejeo hizi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kwamba, Taasisi ya TPRA ime-test baadhi ya pembejeo ambazo zimefika na kukuta kuna changamoto ya baadhi ya kutokidhi vigezo na kwamba pembejeo hizo zirudishwe zilikotoka. Je, Serikali inatuambiaje hizo pembejeo hazitarudi kwa mlango mwingine kwenda kwa wakulima? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maimuna, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu viuatilifu ambavyo vimekuwa na mashaka kwanza nilihakikishie Bunge lako siyo viuatilifu vya msimu wa 2022/2023, bali ni viuatilifu ambavyo vilikuwa procured kwa ajili ya msimu wa 2021/2022 na sasa hivi kama Serikali tulichokifanya, viuatilifu vyote ambavyo vilikuwa vina mashaka juu ya ubora vinakusanywa na kuhifadhiwa katika ghala moja katika Mkoa wa Mtwara chini ya usimamizi wa Serikali. Kwa hiyo nataka nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba viuatilifu hivi havitarudi kwa mlango wa nyuma kwenda kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, kuhusu viuatilifu ambavyo vimeshafika ni ukweli kwamba mwaka jana tulikuwa na tatizo na mwaka jana tenda ilitangazwa mwezi Aprili lakini msimu huu tenda tulizitangaza toka mwezi Januari na mpaka sasa mahitaji ya viuatilifu asilimia 50 ya mahitaji ya viuatilifu vya maji tayari viko Mkoa wa Mtwara na hivi vingine tunatarajia vitafika late tarehe 30 Mei na vitashushwa katika Bandari ya Mtwara.

Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na niwahakikishie wakulima wa korosho, wote watapata viuatilifu vilivyokuwa allocated kwa wakati bila shaka. Pia mwaka huu tumeongeza idadi ya viuatilifu vya maji ili kumpa mkulima matumizi ya viuatilifu vya maji zaidi kuliko matumizi ya sulphur ambayo kwa utafiti wa TARI Naliendele matumizi ya viuatilifu vya maji ni bora zaidi kuliko sulphur na ndomana mwaka huu tumetoa idadi kubwa ya viuatilifu vya maji. Kwa hiyo nataka nimhakikishie Mbunge na wakulima wa korosho kwamba hatutakuwa na matatizo tuliyo experience mwaka jana.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa pembejeo za kilimo wakati wa msimu wa kilimo hususan mbolea. Sasa tunapoelekea msimu wa kilimo, Serikali imejipangaje kupambana na changamoto hiyo? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, changamoto ya msimu uliopita ya upatikanaji siyo suala la availability, tatizo kubwa lilikuwa ni gharama. Mbolea ilikuwepo ndani ya nchi lakini uwezo wa wananchi kununua ulikuwa ndiyo tatizo kubwa. Nataka tu nimwambie Mheshimiwa Mbunge, maelekezo ya Mheshimiwa Rais yako wazi, msimu wa kilimo unaokuja wa 2022/2023, Serikali sasa hivi tuko kwenye majadiliano ndani ya Serikali ili kuona njia ambayo itapunguza bei ya gharama ya mbolea kwa wakulima ili wakulima waweze kuinunua mbolea na waweze kuitumia kwa wakati.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Wakulima wengi ambao wanatumia hivi viuatilifu wanahatari kubwa ya kupata magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo kansa, mtindio wa ubongo na mengine kutokana na kutokutumia ipasavyo viuatilifu hivi. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha inawalinda wakulima kiafya katika matumizi haya ya viuatilifu? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli viuatilifu vikitumika vibaya vinakuwa na madhara kama jambo lolote lile, hata chakula watu wakila vibaya kunakuwa na madhara.

Kwa hiyo tunachokifanya kama Serikali ni kwamba tunatoa mafundisho kupitia Tanzania Plant Health Authority iliyokuwa TPRI huko zamani na baadhi ya mazao sasa hivi tumeanza utaratibu wa ku-train vikundi vya vijana ambavyo vinapewa mafunzo maalum na TPRI na kupewa leseni kwa ajili ya kufanya kazi za kupulizia viuatilifu.

Mheshimiwa Spika, vile vile tumeanza kuwataka wasambazaji wa viuatilifu wanapotengeneza vifungashio watumie lugha ya Kiswahili kutoa maelezo ambayo namna ya mkulima kuchanganya ili iwe rahisi mkulima anaponunua kile kiuatilifu kuweza kufanya kazi ile yeye mwenyewe na kupata mwongozo badala ya kutumia lugha ya Kiingereza ambapo inakuwa ni vigumu kuongoza. Kwa hiyo huo ndiyo utaratibu tumeanza na viuatilifu vyote kuanza sasa vinavyosajiliwa TPRI hata vilivyokwisha sajiliwa na nipitie Bunge lako hili kumwagiza Mkurugenzi Mkuu wa Tanzania Plant Health Authority atekeleze maagizo ya Serikali kwamba viuatilifu vyote vifungashio viandikwe kwa lugha kwa Kiswahili ili mkulima aweze kusoma na kuelewa. (Makofi)
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kumekuwa na tatizo la wakulima kugaiwa kiasi kidogo sana cha viuatilifu ukilinganisha na kile kiasi ambacho kimefika katika maeneo husika.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wakulima wanapata kile kiasi ambacho wanastahili?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea sasa hivi tumeiagiza Bodi yetu ya Korosho, lakini vilevile kwa ajili ya kuweza kupata the light data base ya wakulima na ukubwa wa mashamba yao, tunashirikiana na Halmashauri za Wilaya na Serikali za Mkoa kupitia vyama vyao vya ushirika. Cha kwanza, tunachukua takwimu za uuzaji kupitia vyama vya ushirika ili kumjua mkulima na idadi ya uzalishaji wake.

Mheshimiwa Spika, cha pili, kuanzia msimu wa mwaka 2022/2023 Serikali itatenga fedha kwenye bajeti yetu ya kuzipatia Sekretarieti za Mikoa pamoja na Vyama Vikuu vya Ushirika ili zoezi la usajili wa mashamba ya wakulima na utambuzi wa wakulima liweze kufanyika vizuri ili kujua mahitaji halisi ya pembejeo ambazo wakulima wataigawa.

Kwa hiyo, kuna uwezekano kukaendelea kuwepo kwa changamoto kwa muda, lakini ni jambo ambalo tunalolifanyia kazi. Naamini kwamba ndani ya kipindi cha mwaka mmoja au miwili zoezi la usajili wa utambuzi wa wakulima litakuwa limekamilika na tutaondokana na hili tatizo.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Bei hii inayosemwa imepanda sasa ilikaa zaidi ya miaka mitano bila kupanda, wakati kwenye Soko la Dunia bei ilikuwa ikipanda ukiacha kile kipindi cha Covid-19: Ni upi mkakati wa Serikali sasa angalau kufanya mapitio kila mwaka ili kuhakikisha kwamba tunawasaidia wakulima wa nchi hii wakiwemo wakulima wa Tarafa ya Bungu kule Korogwe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Moja ya njia ya kusaidia kupanda kwa bei ya chai ni kuwa na mnada wa kwetu Tanzania. Mheshimiwa Waziri, Serikali ilituahidi tangu mwaka 2019, ukiwa Naibu Waziri, kuanzisha mnada wa chai Tanzania, lakini mpaka leo mnada huo haujaanzishwa: Ni nini kauli ya Serikali juu ya kuanzisha mnada wa chai ndani ya nchi yetu ya Tanzania?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei iliyodumu kwa kipindi cha miaka mitano ni bei ya shilingi 312. Kikao cha wadau kilichofanyika mwanzoni mwa mwaka huu ndicho tulichobadilisha bei na kuipeleka kuwa shilingi 366 kwa maana ya bei ya chini ya chai. Sasa hivi katika baadhi ya maeneo, hasa maeneo ya Nyanda za Juu Kusini wakulima wanauza chai grade one mpaka shilingi 420. Kwa hiyo, mabadiliko ya bei yamefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ambalo tunalifanya kwenye eneo la bei, Serikali inapitia mfumo mzima wa uchakataji na importation ya chai kutoka nje ili kuvifanya viwanda vya ndani na kuongeza consumption ya matumizi ya chai ya ndani na kuvipunguzia baadhi ya tozo mbalimbali. Mtaona kwenye bajeti itakapokuja Wizara ya Fedha, mtaona mabadiliko katika eneo hilo ili kuvifanya viwanda vya blending vya ndani viweze kutumia zaidi chai ya ndani na kupunguza importation ya chai kutoka nje na kuvitengenezea soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mnada. Nataka nilihakikishie Bunge lako, ni kweli, dhamira ya Serikali toka mwaka 2019 ilikuwa ni kuanzisha mnada, lakini nilihakikishie Bunge lako kwa uwezo wa Mungu, mwaka huu mnada utaanza. Tumeshakamilisha masulala ya miundombinu, tumeshakamilisha eneo la maabara, tumeshakamilisha mwongozo, na sasa hivi tuko hatua za mwisho kwa ajili ya kusajili ma-broker wa Kimataifa ambao watashiriki kwenye trading kwa sababu, uuzaji wa chai una utaratibu wake.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza: -

Je, Serikali inawasaidiaje kwa dharura wananchi wa Kata ya Ruaha Mbuyuni, Wilaya ya Kilolo kwa kuwa wameingia taharuki kubwa sana; mfereji umeacha njia, umehama, intake imeachwa peke yake, maji hayapo kabisa: Wananchi hawali, hawalali, maji hayapo kabisa na mashamba yamekauka?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli eneo la Ruaha Mbuyuni mfereji umehama na mto umehama. Kwa hiyo, hatua ambayo Serikali inachukuwa sasa hivi, timu ya Wataalam wa Wizara ya Kilimo tayari iko Mkoani Iringa kwa ajili ya kuliangalia hilo eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la msingi ambalo nilitaka nilitaarifu Bunge lako na wakulima wa eneo la Ruaha Mbuyuni, tatizo la Ruaha Mbuyuni halitofautiani na tatizo lililokuwepo kwenye maeneo ya Mlenge na Mkombozi. Kila mwaka mvua zikiwa nyingi mto huacha njia. Kwa hiyo, hatua tuliyoamua kama Wizara, tunaenda kulifanyia detailed design na kutangaza baadaye kwa mwaka ujao wa fedha ili ijengwe comprehensive scheme katika lile eneo na tuondokane na hili tatizo la kila mwaka kwenda kufanya repair katika eneo hilo. (Makofi)
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana; je, Serikali ina mkakati gani wa kuweza kudhibiti bei ya kahawa, maana imekuwa ikipanda na kushuka kila mara? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, na siyo tu bei ya kahawa, ni mazao yote bei inapanda na kushuka. Serikali haiwezi kudhibiti bei, bali Serikali jukumu letu la msingi ni kuongeza tija ili kupunguza gharama za uzalishaji ili wakulima waweze kupata faida baada ya gharama zao kupungua. Kwa hiyo, tunachukua hatua mbalimbali za kupunguza gharama za uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, safari hii wakulima wa kahawa wametumia almost asilimia 7.5 ya mbolea yote ya ruzuku iliyosambazwa. Kwa hiyo, ile itawaongezea tija. Mwelekeo wa Serikali ni kuongeza tija kwa kuwapa miche bora ili kuwapunguzia gharama na kuwaongezea uzalishaji waweze kuwa competitive. Hatua ya pili ambayo tunataka kuweka kwenye zao la kahawa ni uhamasishaji wa matumizi ya kahawa ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nchi, tuna-export kahawa kwa wastani wa dola nne, lakini tuna import made coffee kwa wastani wa dola 20. Kwa hiyo, Serikali sasa tunaanza hatua, mtaona kwenye bajeti ya Wizara ya Kilimo, mfano kwenye maeneo ya Kagera tunaanza uwekezaji kwenye Kiwanda cha TANICA ili tuongeze blending na matumizi ya kahawa iliyokuwa processed ndani na kuongeza unywaji wa kahawa ndani ya nchi na kuwaongezea wakulima soko la uhakika na uhakika wa bei.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hali ya hewa ya Tarime na ardhi vinaruhusu kilimo cha zao la chai. Miaka ya nyuma wananchi walikuwa wakilima chai, lakini waliacha kutokana na kutokuwepo na masoko na bei kuwa chini. Sasa kwa mikakati ambayo Serikali imeainisha hapa, nataka kujua, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inahamasisha na kufufua zai la chai kwa Wilaya ya Tarime ili kuweza kukuza uchumi wa wana Tarime? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Tarime ilikuwa ni eneo mojawapo la uzalishaji wa chai na wananchi waliacha. Siyo Tarime tu, hata Mkoa wa Kagera na wenyewe ulikuwa ni eneo mojawapo la uzalishaji wa chai, na Serikali ilibinafsisha baadhi ya maeneo ambayo wawekezaji waliopewa maeneo yale walishindwa kuyaendeleza. Kwa hiyo, kama Serikali sasa hivi, kwa mfano, maeneo ya Kagera tumeanza maongezi na mwekezaji aliyeshindwa ili tuweze ku-take over kile kiwanda kupitia ushirika na Serikali kuweza ku-bail out tuweze kufufua chai eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutafanya tathmini economically, kuangalia kama tuendelee na jitihada tunazozifanya kwenye mazao ya chakula na mazao ya kahawa kwenye eneo la Tarime, ama tulilete zao la chai na litatuathiri namna gani? Kwa hiyo, naomba nitumie nafasi hii kumhakikishia Mbunge tutafanya tathmini and then tutakuwa na majibu ya uhakika. (Makofi)
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nilitaka kujua ni upi mkakati wa Serikali kuhakikisha zao la korosho linarudi katika bei ya miaka ya nyuma ya shilingi 4,000 na kuondokana na bei ya sasa ya kilo shilingi 1,600? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, njia pekee ya mazao ya kilimo kuwa na uhakika wa bei nzuri kwa mkulima na kuwa na uhakika wa soko ni njia mbili. Moja, kuongeza tija, kupunguza gharama za uzalishaji.

Pili, ni kuongeza thamani katika mazao kwa maana ya value addition na kuacha kuuza mazao yetu ghafi nje kwa sababu tunauza na ajira zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie watu wa korosho, kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, 2025/2026 hatuta-export korosho raw, tutabangua zote ndani ya nchi hii. Kuanzia mwaka ujao wa fedha tutatenga kiasi cha Shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kuanza safari ya ubanguaji ndani ya nchi yetu kwa kuwasaidia sekta binafsi ya Kitanzania. (Makofi)
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Moja kati ya sababu zinazowafanya vijana wa Nyanda za Juu Kusini, hususan Mkoa wa Njombe kutokupenda kulima zao hili la chai ni pamoja na bei ya chini ya zao la chai.

Je, ninyi kama Serikali mmejipanga vipi kuhakikisha kwamba mnawa-motivate vijana waweze kushiriki katika kilimo hiki cha chai ikiwa ni pamoja na kuanzisha program za out growers kwenye mashamba ya chai? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli zao la chai siyo vijana peke yake, baadhi ya maeneo wakulima wameanza kuling’oa. Tunapitia upya mfumo mzima wa chai. Ni sahihi kwamba, wakati bei ya chai inapanda ama pale ambapo tunakuwa tegemezi, mfumo wetu wa masoko kwa wenzetu walioko nje ya nchi, maana yake tunakuwa vulnerable siku zote. Kwa hiyo, kama Serikali kama hatua nilizozisema za mwanzo kuanzisha mnada, kuongeza value addition ndani ya nchi, kupunguza importation ya chai kutoka nje, automatically jambo hili litasaidia wakulima kuwa na uhakika wa soko na bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni safari, nawaomba wakulima wa chai nchini, Serikali imeanza kuchukua hizi hatua. Nawaomba wasing’oe chai na wale wote waliouziwa viwanda, hasa nyanda za Kaskazini na baadhi ya maeneo ya Nyanda za Juu, tumewaandikia barua wafufue mashamba na kuviendesha vile viwanda. Kama hawawezi tutafute watu wengine watakaoweza kuwekeza katika maeneo hayo.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa uzalishaji wa tumbaku chini ya uongozi wako mzuri katika Wizara hii umeongezeka sana maradufu mwaka huu; na kwa kuwa, sasa hivi ndiyo tunaenda kwenye soko na uzalishaji ni mkubwa: Serikali imejipangaje kuisaidia Bodi ya Tumbaku kupeleka classifiers kwa wakati kufanya kazi hiyo ili soko lisichukue muda mrefu sana, wakulima waweze kuuza kwa wakati na wapate hela yao kwa wakati? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vita Kawawa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali tunatumia mfumo wa crop financing. Bodi ya Tumbaku ilikuwa inategemea kampuni ziwape magari na mafuta ili kwenda kwenye masoko. Tumetengeneza utaratibu ambao kama bodi, itapata kipato kutokana na zao lenyewe bila kumuumiza mkulima, lakini wakati huo huo kama Wizara tumeanza utaratibu sasa hivi wa kuwatafutia magari Bodi ya Tumbaku ili waweze kufanya kazi zao vizuri na kufanya usimamizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie tu wakulima wa tumbaku na kuwaomba kwa kuwa tumeanza minada sasa hivi, na minada hii imekuwa mizuri, tumbaku imefika mpaka Dola tatu safari hii kwenye minada na ushindani umekuwa wa wazi, nawaomba tu wakulima wahakikishe wanasimamia suala la ubora na wasichanganye kwenye mitumba takataka kwa sababu zitaenda kutuangushia zao letu. Mwaka huu tunatarajia tumbaku itafika tani 120,000 kutoka tani 60,000.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na kwamba zao la korosho limekuwa likiteremka mwaka hadi mwaka, lakini uzalishaji katika Wilaya ya Nanyumbu umekuwa ukiongezeka sana: Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kufikiria kujenga kiwanda ndani ya Wilaya ya Nanyumbu ili kuhakikisha kwamba korosho zote za Msumbiji na zile za Wilaya ya Nanyumbu zinabanguliwa pale pale Wilayani?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kumwahidi Mbunge mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba tutaenda kujenga kiwanda Nanyumbu. Bali, approach ya ubanguaji tunayoendanayo ni private sector driven, na tunaenda kuisaidia sekta binafsi ya kwetu ya Watanzania. Tutaangalia economic reasons za wapi kiwanda kikae. Kama kutakuwa kuna sababu ya kuweka kiwanda Nanyumbu, tutafanya hivyo, wala hatutasita, lakini kwa hatua ya kwanza, Korosho Processing Center tutakayoanza kuijenga, tutaijenga katika Halmashauri ya Nanyamba na Serikali imeshaanza kulipa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama Halmashauri yake inaweza kutenga eneo ambalo tutaanza kuliwekea miundombinu kwa ajili ya baadaye, tuanze huo mchakato sasa hivi, lakini sekta binafsi ndiyo itakayoamua ni wapi inataka kiwanda chake kiwepo, nashukuru. (Makofi)
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Serikali imekuwa na utaratibu wa kuagiza mafuta ya kula nchini, ambayo yameua kabisa soko la mafuta ya alizeti ambayo Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara walihamasisha sana ulimaji wa alizeti. Sasa ni lini Serikali itaacha utaratibu huu ili kulinda bei ya mafuta na alizeti hapa nchini? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli msimu huu kidogo bei ya alizeti imeshuka kwa mkulima. Tunafahamu kwamba mkulima akiuza alizeti chini ya shilingi 900 mpaka ikafika shilingi 700, maana yake anapata hasara. Kama Wizara, tunashirikiana na wenzetu wa Wizara ya fedha kupitia upya maamuzi tuliyoyafanya mwaka 2022 ya ku- reduce tax ya import ya refined palm oil mpaka kufika asilimia 25, kuiangalia impact yake na athari yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nataka niliambie Bunge lako tukufu, import substitution strategy tuliyofanya kama Serikali na ninyi Waheshimiwa Wabunge ya kusaidia kuwekeza kwenye alizeti, ukiangalia report ya BoT ya mwezi huu wa Machi iliyotoka, inaonesha kwa kiwango gani hatua tulizochukua zimepunguza importation ya mafuta ya kula kwa wakati huu wa uzalishaji wa mafuta ya alizeti yameongezeka.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, hatutaruhusu zao la alizeti kufa kwa sababu Serikali inachukua hatua mbalimbali na tutapitia changamoto hizi zilizojitokeza kwa mwaka huu wa fedha ili kuweza kumlinda mkulima na kuhakikisha nchi inajitosheleza mafuta.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Masoko ya Wilaya ya Lushoto hupoteza zaidi ya tani 400 za mbogamboga na matunda kwa kila mwezi. Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kujenga soko kubwa lenye cold room kwa ajili ya kuhifadhi mazao yale au mbogamboga zile ili wananchi wasiendelee kupata hasara?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha kwa kuwapelekea wawezeshaji wakulima wa mbogamboga ili kuongeza mnyororo wa thamani katika mazao yetu haya ya mbogamboga na matunda?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Lushoto na Wilaya za Mkoa wa Tanga, Serikali sasa hivi inafanya tathmini ya kuangalia maeneo ya kujenga masoko, kwa sababu hatutaki kufanya makosa ambayo yamewahi kutokea huko nyuma katika baadhi ya miradi ambapo hata katika wilaya ya Lushoto, kuna jengo lililojengwa la Ubaridi (cold room facility) ambayo mpaka leo haitumiki. Kwa hiyo, nataka nitumie nafasi hii kumwambia Mheshimiwa Mbunge, hivi sasa tunavyoongea wataalam wa Wizara wako Mkoa wa Tanga wakiangalia wapi tuweke masoko ili tuweze kutatua tatizo la mazao ya mbogamboga na matunda hasa machungwa.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Katika Jimbo la Hai kuna wakulima wengi wa mbogamboga wanaolima kwenye mashamba yao binafsi na kwenye vyama vya ushirika, lakini wakulima hao wanaathirika na migogoro iliyopo kwenye vyama vya ushirika. Je, ni lini Serikali itamaliza migogoro kwenye Vyama vya Ushirika Makoa, Mrososangi, Mkundoo, Nkusinde, Byamungo, Narumu na pale Silver Bay ili wakulima hawa waendelee na kazi yao ya kulima?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwenye Chama cha Ushirika cha Kikafu chini, Mrososangi, Mkuu, Chama cha Makoa na baadhi ya vyama vingine na hata Chama Kikuu cha KNCU katika Mkoa wa Kilimanjaro kuna migogoro ambayo inaendelea. Nataka nimhakikishie tu kwamba Mrajisi wa Vyama Vikuu vya Ushirika, hivi sasa tumempa ultimatum kwamba kufikia tarehe 30, Mei awe amemaliza migogoro yote iliyopo na wawekezaji ambao wamekuwa chanzo cha migogoro hii katika vyama hivi. Serikali inaendelea kuchukua hatua za kisheria ili tuweze kuwachukulia hatua za kisheria kwa sababu wao kuwa wawekezaji hatuwezi kuwaruhusu waweze kutumia nafasi hiyo kuweza kuathiri vyama vya ushirika na kuruhusu ubadhirifu unaoendelea katika vyama hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu kwamba Mrajisi wa Vyama Vikuu vya Ushirika anafahamu, kapewa ultimatum na asipochukua hatua za kinidhamu kwa viongozi wa vyama hivi, Serikali itamchukulia yeye hatua na tutamshauri Mheshimiwa Rais amwondoe katika nafasi hii kwa sababu nafasi aliyonayo ni ya uteuzi wa Mheshimiwa Rais.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kumekuwa na changamoto sana kwenye suala la masoko hasa katika kilimo cha zao la parachichi na wakulima wamekuwa wakihangaika wenyewe. Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kuna soko la uhakika katika zao hili la parachichi ambalo litaleta Tanzania pesa nyingi za kigeni?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester, Mbunge wa Viti Maalum na mkulima wa parachichi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli kwamba parachichi ni moja zao ambalo linakuwa kwa kiwango kikubwa na hivi sasa kama Serikali tuko katika hatua za mwisho tukishirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara kufungua Soko la China ambalo ni soko la uhakika. Vile vile, Waheshimiwa wataona kwamba Serikali imefanya kazi kubwa ya kufungua masoko mengi katika zao la parachichi. Mwaka huu 2023 zao la parachichi export imeongezeka kutoka katika tani 8,000 mpaka tani 29,000. Kwa hiyo, sisi kama Serikali tunaendelea kuchukua hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ambayo inawakabili wakulima wa parachichi sio soko tu, ni miundombinu ya uhifadhi na miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo hayo. Nataka tu niwahakikishie kwenye bajeti mwaka kesho 2024/2025, mtaona mwaka huu 2023/2024 tunaanza kujenga common use facility, lakini mwaka 2024/2025, katika bajeti ya Wizara ya Kilimo kutakuwa na program mpya ya kuwasaidia wakulima 10,000, kuwachimbia visima na kuwapa irrigation kit za Hekta moja kwa kila mtu ili aweze kuweka katika shamba lake. Kwa hiyo Serikali inaendelea kufanya kazi hizo.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naishukuru sana Serikali kwa majibu hayo mazuri pamoja na majibu hayo mazuri bado nina maswali ya nyongeza. Wahanga waliozulumiwa pesa zao katika Jimbo la Muhambwe ni Lugongwe AMCOS, Chapakazi AMCOS, Amani AMCOS na Migwezi AMCOS ambao hawa waliingia mikataba na JESPAN baada ya kuwa wamejiridhisha kwamba Serikali imewapatia vibali hawa JESPAN.

Je, Serikali aioni iko ukunimu wa kulipa hizi pesa kwa sababu wao ndiyo waliyowadhamini hawa wakulima halafu wenyewe Serikali itaendelea na hizo kesi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa makampuni haya ya wazawa yanawazulumu hawa wakulima hii JESPAN ni mfano tu. Serikali imejipanga vipi kuyadhibiti haya makampuni ili wakulima wetu wasiendelee kudhulumiwa? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli makampuni haya tumeanza kuchukua hatua za kisheria, baadhi ya makampuni yanatoa huduma kwenye sekta ya tumbaku baadhi yao tumeishayakata fedha kupitia TCJE kama dola lakini nne ambazo walitoa huduma ili tuweze kuzirudisha kwa wakulima. lakini hatua ya pili ni kwamba Serikali inapompa leseni kwenda kufanya biashara anapokwenda kinyume kuna utaratibu wa kisheria na kwake yeye kupewa leseni ya kwenda kufanya biashara haina maana ile responsibility siku ya mwisho itahamia kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tabia ya wakulima kudhulumiwa na wafanyabiashara na hii haipo tu kwenye tumbaku, ipo kwenye pamba, ipo kwenye korosho, ipo kwenye maeneo mengi, na wizi mwingine hushirikisha vyama vya ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano kesi iliyoko Mkoa wa Katavi chama cha ushirika kimeshirikiana na Kampuni ya NEIL kuweza kuwaibia wakulima. Kwa hiyo, tunachukua hatua za kisheria niwaombe Waheshimiwa Wabunge wa Sikonge Wilaya ya Sikonge Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Tabora na Wilaya ya Chunya wa tumbaku waliyopata madhara mwaka 2019/2020 niwahakikishie kwamba Serikali inachukua hatua na tutamaliza haya matatizo na yamekuwa fundisho kwetu ndiyo maana tumewaondoa wanunuzi wa namna hii na tunakuja na sheria ya kilimo itakayoweza ku–criminalize wizi unaofanyika kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na majibu ya Serikali. Naomba kutumia nafasi hii kwanza kuipongeza Serikali, kwa maana ya Wizara ya Kilimo na Wizara ya Wizara ya Mambo ya Nje kwa programu hii ya kuwajengea vijana uwezo na mafunzo ya ziada, na pia kuipongeza Serikali hususan Wizara ya Kilimo kwa kuwajumuisha hawa vijana 79 katika programu ya BBT. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza: Kwa kuwa vijana hawa tayari walishasoma vyuo vikuu na vyuo vya kati na wakapata ujuzi wa ziada huko Israel; je, Serikali kwa maana ya Wizara ya Kilimo iko tayari sasa pamoja na kuwahusisha kwenye BBT kuanzisha hiyo programu ya mashamba makubwa (block farming); na kwa kuwa tayari wenyewe ujuzi wanao; na tayari hawa 79 wanatumika kule lakini hawa waanze kabisa kazi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa sababu Serikali imetenga fedha nyingi na inajenga miradi mingi ya umwagiliaji ambayo bila shaka itahitaji wataalam katika kuiendesha katika kuwasaidia wakulima wetu; je, Serikali iko tayari kuwatumia baadhi ya vijana hawa kwa mfumo hata wa kuwalipa japo posho ya kujikimu ili wawasaidiwe wakulima wetu katika hii miradi mikubwa ambayo imetekelezeka hususan kule Mtura?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza vijana wote ambao wanaenda Israel kwenye sekta ya kilimo mazao, wapo wengine ambao hawaendi kwenye sekta ya kilimo mazao; wengine wanaenda kwenye mifugo na maeneo ya namna hiyo. Kwa hiyo, wale ambao wako kwenye sekta ya kilimo mazao, tumeanza kuwa- incorporate kwenye programu ya BBT kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi. Wapo ambao tayari wanafanya shughuli za kilimo ambapo tumeanza kuwatambua sasa hivi, wanafanya shughuli za uzalishaji katika maeneo yao na tumewaingiza kwenye component ya pili ya programu ya BBT ya kuwapa grants na mikopo nafuu ya asilimia 4.5. Kwa hiyo, tumeshaanza kuwatambua na kuwaangalia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kuwatumia kama extensional officers, nilitaka tu niliambie Bunge lako tukufu kwamba, kuanzia mwaka ujao wa fedha na tutakapoleta mabadiliko ya Sheria ya Umwagiliaji na Ugani hapa ndani ya Bunge lako, tunaangalia namna ya kuwatumia vijana waliopo mashuleni kwenye programu za extension ambao wanafundishwa katika vyuo vyetu vya kilimo. Vile vile vijana ambao wana utaalam wa kilimo ili kuanza kuanzisha kampuni binafsi za extension services kwa wakulima na waweze kutoa huduma za namna hiyo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi. Naishukuru Serikali kwa majibu. Je, Serikali haioni kuwa sasa shule zetu za sekondari za kata zimekuwa na wanafunzi wengi wasiopata kuendelea na masomo ya juu na kwa hiyo, vijana hao wangekuwa sehemu moja ya kuwajengea uwezo wale wanafunzi walioko shuleni kwa kuanzisha mashamba madogo ya majaribio na mafunzo katika shule hizo katika kanda na wilaya zetu? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kuna mchakato unaendelea wa mapitio ya sera ya elimu, nami naishukuru Wizara ya Elimu kuweza kuchukua component ya agriculture kuwa sehemu ya mapitio haya ya sera. Mawazo kama haya tutaendelea kuyapokea na siwezi kutoa commitment sasa hivi kwamba tutaanza kuweka mashamba darasa katika kila sekondari, lakini ni wazo na ninashukuru, nasi kama Serikali tumelipokea.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa mafanikio makubwa ya kilimo Israel ni yale ya Kibbutz Farms na vijana wa kitanzania waliofanikiwa nadhani hayo ndiyo pia wanaenda kujifunza: Je, Serikali iko tayari sasa kutumia vijana hao kuwarejesha katika maeneo yao ya vijijini kwa sababu Watanzania wengi na karibu wote ni wakulima wadogo wadogo ili wanufaike?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mama Shally Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye majibu ya msingi na maswali aliyouliza Mheshimiwa Cosato, namna ya kuwatumia vijana hawa ni lazima tuwe na mfumo wa ugharamiaji kwa sababu huwezi kutaraji kumpeleka kijana kijijini ukamwambie akatoe elimu bila kuwa na mfumo wa ugharamiaji.

Mheshimiwa Spika, tumepokea mawazo ya Waheshimiwa Wabunge na wadau wengi wa sekta ya kilimo namna ya kuwatumia vijana walioenda Israel, walioenda nje lakini wapo vijana ambao wamesoma katika vyuo vyetu, wamesoma kilimo na wana utaalam wa kilimo cha kisasa, lakini bado wapo mtaani. Kwa hiyo, kama Wizara, tunapoenda kupitia mapitio ya sheria ambayo tutaileta ndani ya Bunge lako tukufu ya Irrigation and Extension Services, tuta-incorporate component ya vijana ambao wana elimu ya extension namna ambavyo watatumika na namna gani tutakuwa na mfumo mzuri wa ugharamiaji wa huduma zao.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Wilaya ya Kahama haijanufaika na mradi wa BBT; na kwa kuwa Halmashauri ya Msalala sasa tuko tayari kupokea mradi huu kwa vijana wetu: Je, ni lini sasa Mheshimiwa Waziri utafika katika Halmashauri ya Msalala ili tuweze kuanzisha mradi huu? Ahsante.
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Iddi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza Wizara iko tayari kushirikiana na Halmashauri yoyote katika nchi yetu ambayo iko tayari kutenga eneo la kilimo kwa ajili ya mfumo wa block farm na kwa ajili ya mfumo wa BBT. Mfano mzuri ni Halmashauri ya Makete ambao wameamua kutenga ten percent yao kuwakopesha vijana, na sisi Wizara tukawapatia pembejeo kwa maana ya mbegu za bure kwa ajili ya kilimo cha ngano. Kwa hiyo, nihamasishe Waheshimiwa Wabunge ninyi ni wajumbe wa Baraza la Madiwani, ni wajumbe wa Kamati za Fedha tengeni maeneo na kuwa tayari kutenga sehemu ya asilimia kumi za Halmashauri kuwasaidia vijana katika maeneo yenu, na Wizara tuko tayari kuja ku-support initiatives za namna hiyo. (Makofi)
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuwa nchi yetu imejaliwa wahitimu wengi wa vyuo vikuu kila kona wakiwemo kule Nachingwea. Je, Serikali inachukua vigezo gani kuwapeleka

hawa vijana wetu ambao wametapakaa nchi nzima huko Israel? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, cha kwanza hii programu inakuwa coordinated na Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje kwa kushirikiana na taasisi ya Ministry Affairs ya Israel for International Development and Corporation. Mara nyingi Serikali huwa inatoa window na huwa kuna utaratibu maalum ambao unatumika namna ya kuwapata vijana wanao-apply na kuweza kwenda kushiriki katika windows za namna hii.

Mheshimiwa Spika, tumekutana na ubalozi wa Israel hivi karibuni na kujadiliana nao namna ya kuboresha huduma ya kuwapata vijana, kwa sababu wapo vijana ambao wana apply kwa ajili ya kwenda kufanya jambo A, wakifika kule wanajikuta wamekuwa committed kufanya jambo lingine tofauti na kile ambacho walitarajia. Tumeongea na Ubalozi wa Israel, tunaendelea nao na mazungumzo tukishirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje, badala ya kuwasafirisha hao vijana. Tunavyo vituo vingi katika nchi yetu. Ushirikiano ule wa utalaam tuweze kuutumia ndani ya nchi na waweze kuja kutusaidia ndani ya nchi yetu. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri na naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tarehe 8 Agosti huwa ni siku ya wakulima nchini, na siku hiyo wakulima wengi hupata fursa ya kukutana kuonesha maonesho na kujifunza, na kwa kuwa Serikali imesimamisha haya maonesho karibu mwaka mmoja na nusu sasa.

Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na kusimamishwa Maonesho haya ya Nanenane nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa kumekuwa na vikwazo vingi sana barabarani kwa magari yanayosafirisha bidhaa hizi za mazao yanayoharibika kama nyanya, parachichi na kadhalika na kusababisha hasara kubwa sana kwa wakulima.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kutoa vibali maalum kwa ajili ya magari yanayosafirisha mazao haya kwa saa 24, kwa sababu kuna magari makubwa ambayo yanazuiwa, saa 12 yanaambiwa yasisafirishe mazao kupeleka hata nje ya nchi kama South Africa? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, zao la parachichi na mfumo mzima wa parachichi katika nchi yetu haukuwa na mwongozo. Kwa hiyo Serikali sasa hivi iko kwenye hatua za mwisho na tutazindua mwongozo wa kusimamia zao la parachichi kuanzia shambani mpaka sokoni na utaratibu wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kupitia Bunge lako tukufu wakati tunafanya mawasiliano ndani ya Serikali kati ya Wizara ya Kilimo, TRA na watu wa TANROADS kwa maana ya Wizara ya Miundombinu ili ku-develop stika maalum ambazo zitasimamia mazao ya horticulture, magari yote yanayobeba mazao ya horticulture yatakuwa na stika maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nipitie Bunge lako tukufu kuziomba Mamlaka za Serikali za Mitaa kwamba mazao ya parachichi na mazao ya mbogamboga ni perishable, ni vizuri kutokuweka vikwazo visivyokuwa na ulazima barabarani kwa kipindi hiki ambacho tunaandaa mwongozo ambao utasimamiwa ndani ya Serikali katika ngazi zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo huu utaratibu wa kuwazuia kusafiri usiku nadhani siyo sahihi na ninapenda kupitia Bunge lako tukufu kuwaomba viongozi wa mikoa wa-facilitate transportation ya mazao ya kilimo hata kama ni usiku namna gani. Kama mtu anasafiri aendelee na kusafirisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kipengele cha pili kuhusu Nanenane; ni kweli Serikali ilisimamisha Nanenane kwa muda, na ninataka kupitia Bunge lako tukufu kuwatangazia Watanzania na wakulima kwamba Nanenane tunarudisha na mwaka huu Kitaifa itafanyika Mkoa wa Mbeya. Serikali iko kwenye kufanya total reform ya mfumo wa Nanenane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ningepitia Bunge lako tukufu kuzitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa; shughuli za Nanenane zitasimamiwa na Wizara ya Kilimo na sekretarieti za mikoa. Taasisi iliyokuwa inaitwa TASO ambayo ilikuwa imejimilikisha kusimamia Nanenane haitahusika na wala haihusiki na masuala ya Nanenane na viwanja vya Nanenane. Suala hili litasimamiwa na Serikali, Wizara ya Kilimo na Mamlaka za Mikoa kwa maana ya mikoa husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali sasa hivi tuko kwenye hatua za mwisho za kuandaa mfumo mpya wa shughuli za Nanenane, na Tanzania tutakuwa na kitu tunaitwa Tanzania International Agricultural Trade Show ambapo tutakuwa na eneo moja ambalo nchi nzima kila mwaka kimataifa litakuwa linafanyika hapo na mikoa itakuwa inafanya shughuli za kikanda. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku za karibuni kumekuwa na taarifa ambazo zimekuwa zikitapakaa kwenye mitandao pamoja na picha zikionesha kwamba parachichi ya Tanzania haikidhi viwango, jambo ambalo siyo kweli. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na suala hili? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwahakikishie Watanzania na niwahakikishie wateja wote wanaonunua parachichi za Tanzania kuwa parachichi za Tanzania zinakidhi vigezo vya kimataifa na ndiyo maana tumekuwa sasa hivi tukifungua masoko mapya na hivi karibuni tumefungua soko la India, na ni Tanzania pekee ambayo imepata import duty exemption ya parachichi yake katika soko la India, hili ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; tunazo international certification institutions ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, parachichi yetu inapotoka nje ya mipaka inakuwa na certifications za kimataifa zote ambazo zinakubalika katika soko la dunia. Kumekuwa na tatizo la competitors wetu na mimi nataka niwaombe exporters wa Tanzania wahakikishe wanapo-export parachichi ya Tanzania inaondoka na trademark iliyoandika Produce of Tanzania ili kuweza kui-protect image ya parachichi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushindani upo, watu watataka ku-distort image yetu. Niwaombe Watanzania, yeyote anayepata taarifa yenye mashaka kuhusu product ya Tanzania awasiliane na Wizara ya Kilimo na sisi tutakuwa tayari kui-protect bidhaa yetu popote pale.