Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu (63 total)

MHE. KANGI A. N. LUGOLA aliuliza:-
Mapambano dhidi ya uvuvi haramu katika Bahari ya Hindi yamekuwa yakihusisha njia ya kuwanyang‟anya zana haramu wavuvi wadogo kupitia mradi wa MACEP na kuwapatia zana za uvuvi zinazoruhusiwa:-
(a) Je, mradi huo umefanikiwa kwa kiwango gani?
(b) Kama umefanikiwa; je, ni lini mradi huo utaanzishwa kwa wavuvi wadogo wa Jimbo la Mwibara katika Ziwa Victoria?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kangi Lugola, Mbunge wa Mwibara kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa usimamizi wa mazingira ya Ukanda wa Pwani na Bahari Marine and Coastal Environment Management Project (MACEMP) ulitekelezwa mwaka 2005/2006 hadi 2012/2013 katika Halmashauri 16 za Ukanda wa Pwani upande wa Tanzania Bara na Halmashauri kumi kwa upande wa Tanzania Zanzibar. Lengo la mradi huu lilikuwa kuimarisha usimamizi na matumizi ya rasilimali za uvuvi katika Bahari Kuu na kuinua hali ya maisha za jamii hizi za Pwani.
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi wa MACEMP umekuwa na mafanikio kadhaa ikiwemo kuimarisha usimamizi wa rasilimali na uvuvi katika Ukanda wa Pwani kwa kuanzisha mamlaka ya usimamizi na uvuvi katika Bahari Kuu yaani (Deep Fishing Authority) kuwepo kwa mtambo wa kufuatilia mwenendo wa meli pamoja na kuwezesha kununuliwa kwa boti 16 za doria. Lakini pia kumekuwepo na kuwezesha uendeshaji wa doria katika nchi kavu na anga na kuwezesha kuanzishwa kwa vikundi 182 vya usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi, yaani Beach Management Units (BMUs). Pia vikundi 47 vyenye wavuvi 193 na wavuvi 436 kutoka katika Hifadhi ya Bahari za Mafia na Mtwara walipatiwa zana za uvuvi na kuondokana na matumizi ya zana haramu.
Vilevile mradi umewezesha jamii za Pwani kuibua miradi midogo 470 ya kiuchumi yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 6.6 ambayo ililenga kuboresha maisha ya Jamii hizo na kunufaisha wananchi wapatao 8000. Aidha, mradi uliwezesha ujenzi wa mialo mitatu ya kisasa ambayo ni pamoja na mwalo wa samaki Kilindoni ulioko Mafia, Masoko ulioko Kilwa na Nyamisati ulioko Rufiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba muda wa kutekeleza mradi wa MACEMP umemalizika na Serikali itatekeleza miradi yenye malengo kama hayo katika maeneo mbalimbali ikiwemo Mwibara kutokana na uwezo wa Serikali. Miradi yenye malengo sawa na MACEMP imekuwa ikitekelezwa katika Ukanda wa Ziwa Victoria ambayo ni pamoja na Mradi wa Utekelezaji wa Mpango wa Usimamizi wa Uvuvi katika Ukanda wa Ziwa Victoria uliotekelezwa mwaka 2003 hadi Agosti, 2010 ambao umesaidia ukuaji na uendelezaji wa uchumi katika Ukanda huo na rasilimali za uvuvi zilizoko katika Ziwa Victoria.
Pili, Mradi wa Usimamizi wa Mazingira Ziwa Victoria wa Awamu ya Kwanza na ya Pili na Tatu kumekuwepo na utekelezaji wa pili ambao ulitekelezwa hadi mwaka 2005 na kwenda hadi mwaka 2013 ambao ulikuwa na malengo hayo hayo. Mradi huu umewezesha kuimarika kwa usimamizi wa matumizi endelevu ya rasilimali za uvuvi na kuongeza ajira na kuboresha huduma za uvuvi katika jamii hizo zinazozunguka Ukanda wa Ziwa Victoria.
MHE. HAMIDU H. BOBALI aliuliza:-
Wakulima wengi Mkoani Lindi wameamua kujikita katika zao la ufuta ambalo ndilo zao la biashara:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wakulima hao kupata pembejeo kupitia Mfuko wa Pembejeo.
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamidu Bobali Mbunge wa Mchinga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa zao la ufuta ambalo linalimwa kibiashara katika Mikoa ya Kusini yaani Lindi, Mtwara na Ruvuma na maeneo mengine tangu mwaka 1940. Mikoa hiyo huzalisha zaidi ya asilimia 75 ya ufuta wote unaozaishwa hapa nchini. Ufuta, hutumika kama chakula kwa binadamu, na vilevile hutumika kama chakula kwa mifugo.
Mheshimiwa Naibu Spika, zao la ufuta hustawi zaidi kwenye ardhi yenye rutuba ya asili na kwamba kiasi kidogo cha mbolea ya chumvichumvi, kinahitajika ndiyo maana wakulima hupendelea zaidi kulima kwenye ardhi mpya kwa kila msimu. Hata hivyo, ili kupata mavuno mengi, inahitaji kiasi kidogo cha mbolea za kupandia na kukuzia, na hivyo kulingana na hali ya udongo katika eneo husika kunahitajika mbolea .
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mpango wake wa ruzuku kwa wakulima inaangalia uwezekano wa kuongeza mazao mengine ikiwemo ufuta pale bajeti itakaporuhusu. Hata hivyo, kwa kuwa wakulima wa Mkoa wa Lindi wameamua kulima ufuta kama zao lao la bishara, Serikali inawashauri Wakulima wa Mkoa wa Lindi kupitia kwenye vikundi vyao vya ushirika kuomba mikopo kwenye Mfuko wa Taifa wa Pembejeo ili kuweza kujihakikishia upatikanaji wa pembejeo na kwa namna ya soko huria.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza:-
Lini Serikali itatatua kero ya pembejeo za kilimo kutofika kwa wakati katika Kata za Kipengele, Wangama, Igima, Ulemwe na Makoga?
WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ucheleweshaji wa pembejeo kwa wakulima unasababishwa na baadhi ya mambo kama haya yafuatayo:-
La kwanza, ni mawakala kutokulipwa kwa wakati kutokana na uhaba wa fedha na hivyo kuwapunguzia uwezo wa kutoa huduma hiyo kwa wakati.
Pili, utaratibu au mchakato mzima unaofanya mpaka mkulima apate vocha au pembejeo ni mrefu na hivyo huchukua muda mwingi na kuchangia kuchelewa kwa pembejeo. Serikali inaangalia jinsi ya kurahisisha utaratibu huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika msimu wa mwaka 2015/2016 imetumia makampuni ya pembejeo za kilimo kuteua mawakala wa kusambaza pembejeo kwa wakulima. Kupitia utaratibu huu, mawakala waliteuliwa na makampuni badala ya Kamati za Pembejeo za Wilaya ili kuokoa muda wa pembejeo kuwafikia wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wanufaika wa vocha za pembejeo, Wizara ilikabidhi vocha za pembejeo kwa Mkoa wa Njombe tarehe 4/11/2015 na kwamba Mkoa ulikabidhi Wilaya ya Wanging’ombe tarehe 6/11/2015 na Kata ya Igima ilipokea vocha tarehe 9/11/2015. Kata ya Kipengele, Wangama, Ulembwe, Kidugalo, Imalinyi, Igosi na Makoga zilipokea vocha za pembejeo tarehe 10/11/2015.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia tarehe 20/11/2015 huduma ya usambazaji wa pembejeo ilianza kutolewa na mawakala walioteuliwa na Makampuni ya Pembejeo ili kuwahi msimu wa kilimo ambao huanza kati ya mwezi Oktoba na Novemba.
Wizara ya Kilimo na Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Mikoa na Halmashauri za Wilaya tunaendelea kuhamasisha Makampuni na mawakala wa pembejeo kufikisha pembejeo kwa wakulima kwa wakati kabla ya msimu haujaanza.
MHE. PASCAL Y. HAONGA aliuliza:-
Shirika la NAFCO Magamba limeshindwa kuyaendesha mashamba yaliyochukuliwa kutoka kwa wananchi na kuwakosesha maeneo ya kulima na mara nyingine kuwakodishia kwa gharama kubwa.
Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka wa kuyarejesha mashamba hayo kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pascal Yohana Haonga, Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa, kwa sasa Serikali haiwezi kulirejesha shamba hilo kwa wananchi kwa kuwa lipo kimkakati kwa ajili ya kuongeza upatikanaji wa mbegu za kutosha ili kukidhi mahitaji ya mbegu nchini. Vilevile kupitia shughuli za uzalishaji mbegu, wakulima hupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mbolea na madawa ya kilimo na utunzani wa shamba, pia kusambazia teknolojia mpya za kilimo bora.
Aidha, tayari Serikali ilichukua hatua za kurejesha mashamba nane ya kahawa ya Ngamba, Shishiwanda, Ihanda, Ndugu I, Ndugu II, Tukumbi, Ruanda na Ishera ambayo yalikabidhiwa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ili kuyagawa au kuyauza kwa wananchi kwa shughuli za kiuchumi na kijamii ambapo baadhi yao wamepatiwa hati miliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Kilimo Mifugo na Uvuvi, tayari alishatembelea shamba hilo, akiwa pamoja na Mkuu wa Mkoa, Mbunge wa Mbozi mwenyewe, wataalam wa ASA na wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi. Katika ziara hiyo, wataalam wa ASA na Halmashauri walitoa maelezo kuwa kuna kipindi cha kupumzisha shamba kwa mwaka mmoja au miwili ili kuongeza rutuba ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taratibu hizo za kitaalam zinaweza kutafsiriwa kuwa shamba hilo halitumiki ipasavyo. Aidha, baada ya ASA kukabidhiwa shamba hilo na Shirika Hodhi la CHC, hakuna wakulima waliowahi kukodishwa shamba hilo, bali ASA imekuwa ikishirikiana na sekta binafsi katika uzalishaji wa mbegu kwenye shamba hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati uliopo wa kuzalisha mbegu ni pamoja na kupanua wigo wa ushirikiano ili Kampuni zaidi zishiriki katika uzalishaji wa mbegu kwa kutumia shamba hili. Vilevile kuhamasisha vikundi vya vijana ili washirikiane na ASA katika uzalishaji wa mbegu. Mwisho, kuweka miundombinu muhimu iliyohitajika katika uzalishaji ikiwemo kuunganisha umeme wa gridi na kujenga miundombinu ya umwagiliaji.
MHE. SUSANNE P. MASELLE aliuliza:-
(a) Je, Serikali imechukua juhudi gani za makusudi kudhibiti vitendo vya kubambikizia watu kesi vinavyofanywa na baadhi ya askari wasiokuwa na maadili?
(b) Je, Serikali itakuwa tayari kuanzisha kitengo cha siri ndani ya Jeshi la Polisi kitakachoshughulikia adha hii?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Susanne Maselle, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa mujibu wa sheria, kanuni, miongozo pamoja na taratibu na wale wanaobainika kukiuka maadili ya Jeshi, huchukuliwa hatua kwa kuwashitaki kijeshi kwa mujibu wa PGO 103 na 104 kwa kuwapa adhabu mbalimbali ikiwepo kuwafukuza kazi anaobainika kukiuka maadili ya Jeshi ikiwemo kubambikia watu kesi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imefanya jitihada za kuanzisha Kitengo cha Malalamiko katika ngazi ya Makao Makuu, Mikoa na hata Wizara ili kutoa mwanya kwa mtu yeyote anayeona kuwa ameonewa, kuwasilisha malalamiko yake na malalamiko hayo kushughulikiwa. Hata hivyo, raia wanayo haki ya kulalamika katika vyombo vingine vya kisheria wanapoona hawatendewi haki kwa mujibu wa sheria za nchi.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi limeweka wazi utaratibu wa namna ya kuwashughulikia askari wasio waaminifu, hivyo halitakuwa tayari kuanzisha kitengo cha siri kwa kazi hiyo kwani utaratibu uliopo unashuhudia na umekuwa na mafanikio.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, siku za usoni kama hivyo ilivyo kwa mikoa michache hapa nchini ambapo kazi ya polisi itabaki kuwa ni ya kupeleleza kesi na mwenye mamlaka ya kupeleka kesi mahakamani ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali. (Makofi)
MHE. HASNA S. K. MWILIMA aliuliza:-
Gereza la Ilagala limehodhi eneo kubwa la shamba na kufanya wananchi wa Kata ya Ilagala kukosa maeneo ya kulima.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kutoa sehemu ya eneo kwa ajili ya wananchi wa Ilagala ili na wao waweze kupata maeneo ya kulima?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Katunda Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Gereza la Ilagala ni gereza la kilimo na mifugo ambapo linamiliki jumla ya ekari 10,760 na kati ya ekari hizo, ekari 4,500 ziko katika milima na mabonde ambapo zimehifadhiwa kwani ni vyanzo vya mito katika eneo hilo. Ekari 3,000 zimetengwa na zinatumika kwa ajili ya ufugaji wa ng‟ombe, mbuzi na kondoo; na ekari 5,000 kwa ajili ya makazi na ekari 2,760 ni kwa ajili ya kilimo cha mazao ya mahindi; mahindi ya mbegu, michikichi, mihogo, mbaazi, mboga pamoja na matunda. Hata hivyo, pamoja na shughuli tajwa hapo juu, eneo hilo bado halitoshelezi kwa ajili ya mahitaji yaliyokusudiwa.
MHE. HAMADI SALIM MAALIM aliuliza:-
Je, ni kwa nini Askari wa Jeshi la Polisi hucheleweshwa maslahi yanayoendana na vyeo vyao pindi wanapomaliza mafunzo kwa ngazi mbalimbali kama vile Koplo, Sajent, Staff Sajenti, Meja na vingine?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamadi Salim Maalim, Mbunge wa Kojani, kama ifuatavyo:-
Kwanza nikiri, ni kweli kumekuwepo na matatizo ya Askari kupanda vyeo na kucheleweshewa malipo yanayoambatana na kupanda vyeo hivyo. Askari Polisi kupanda vyeo kama ilivyo kwa watumishi wengine wa umma na vyeo hivyo kuambatana na kuongezeka kwa maslahi kulingana na cheo walichopandishwa. Kwa mwaka 2014/2015, jumla ya askari 1,657 wa Vyeo vya uongozi mdogo walipandishwa vyeo mbalimbali na mwaka 2015/2016, Askari wapatao 3,017 walikuwa katika Vyuo vya Polisi wakihudhuria mafunzo na hivyo kupandishwa vyeo kuwa maafisa na wakaguzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwepo na ucheleweshaji kama nilivyosema wa mafao haya yanayolingana na vyeo walivyopanda kijeshi na Serikali mara zote imekuwa ikijitahidi kurekebisha mishahara ya vyeo vipya kwa haraka iwezekanavyo kwa askari waliopanda vyeo. Yapo matatizo ya kiufundi yanayojitokeza wakati wa zoezi la kurekebisha mishahara na kutokea baadhi ya askari kutorekebishiwa mishahara yao na hivyo juhudi hufanyika ili kutatua tatizo hilo mara moja na mhusika anapowasilisha malalamiko yake Polisi ama Makao Makuu.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza:-
Kumekuwa na uuzaji holela wa vifaa hatarishi barabarani kama vile visu, mapanga na kadhalika.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kukomesha biashara hii ambayo ni hatari kwa usalama wa wananchi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na uuzaji holela wa vifaa hatarishi barabarani. Vifaa hivi hutumika kwa shughuli mbalimbali kama vile kilimo. Hata hivyo vinaweza kutumika vibaya na kuhatarisha maisha ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri kwa Halmashauri zetu zote na mamlaka zinazohusiana na biashara kutenga maeneo maalum na kusimamia vema biashara hizo. Aidha, kama hali hii itaendelea Serikali haitasita kuchukua hatua stahiki kukomesha biashara ambayo inaweza ikaleta hatarishi pindi itakapotumika vibaya.
MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-
Baadhi ya watumishi wa DEPU mwaka 1999 – 2000 na Idara ya Uhamiaji hawajapandishwa vyeo mpaka sasa, licha ya kuwa na vigezo kama vya elimu na ngazi ya shahada huku wenzao wakiwa wamefikia vyeo vya Makamishna na Kamishna wasaidizi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia watumishi kupata haki yao ya vyeo stahiki kama ilivyo kwa wenzao waliopandishwa vyeo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Salum Pondeza, Mbunge wa Chumbuni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wa Idara ya Uhamiaji walioajiriwa mwaka 1999 – 2000 walikuwa na viwango tofauti vya elimu kama vile wengine wakiwemo kidato cha nne, wengine wa kidato cha sita, stashahada na wengine wakiwa na shahada. Katika watumishi wote hao hakuna aliyekuwa amefikia cheo cha Kamishna au Kamishana Msaidizi kama Mheshimiwa Mbunge alivyouliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi hao kwa sasa wametofautiana vyeo kutokana na sababu zifuatazo:-
Moja, waliajiriwa katika vyeo tofauti kulingana na elimu zao wakati wanaajiriwa na kujiunga katika mafunzo ya awali ya uhamiaji.
La pili; baadhi yao walijiendeleza kielimu wakati wapo katika ajira ili kuinua viwango vyao vya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuchukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria na kupelekea wengine kusimamishwa kupata vyeo kama ambavyo iko kwenye Sheria za Utumishi wa Taasisi hii.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-
Askari Magereza katika Mji wa Tarime wamekuwa wakilalamika kuwepo kwa mlundikano wa mahabusu ndani ya Gereza la Mji wa Tarime. Hii inatokana na mlundikano wa kesi ndani ya Mahakama ya Wilaya kwa kigezo cha upelelezi kutokamilika:-
(a) Je, kwa nini kesi zenye vigezo vya dhamana watuhumiwa wasipewe dhamana ili kupunguza mlundikano wa mahabusu na gharama kwa Serikali?
(b) Je, nini mkakati mahususi wa Serikali katika kuhakikisha Jeshi la Polisi linamaliza upelelezi kwa wakati ili kuweza kupunguza mlundikano?
(c) Je, ni hatua gani zinachukuliwa kwa Askari Polisi ambao wanawabambikia kesi wananchi na kupoteza nguvu kazi za Taifa kwa kuwafanya wananchi waishi Gerezani?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi nchini, chini ya Kifungu 64 cha Sheria na Mwenendo wa Makosa ya Jinai limepewa mamlaka ya kutoa dhamana kwa baadhi ya makosa kabla washtakiwa kufikishwa Mahakamani. Mara nyingi mahabusu wanaendelea kukaa magerezani licha ya makosa yao kuwa ya dhamana kwa kushindwa kukamilisha masharti chini ya Kifungu 148(5), (6) na (7) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20 na masharti mengine yanayotolewa na Mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutoa mafunzo ya upelelezi ya muda mfupi na muda mrefu nje na ndani ya nchi ili kuwajengea weledi wapelelezi na kufanya upelelezi kufanyika na kukamilika kwa wakati. Aidha, Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa na Wilaya wanaendelea kuboresha mifumo ya usimamizi wa upelelezi na kukagua mafaili mara kwa mara ili kujionea mwenendo wa kesi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa siyo kweli kwamba Askari Polisi hukumbatia kesi za wananchi. Uhaba wa vitendea kazi vya uchunguzi ambavyo hupatikana Makao Makuu tu, vile ambavyo ni vya kisayansi kuchelewa kupatikana kwa majibu ya uchunguzi wa kisayansi kutoka vyombo vingine, ni baadhi ya sababu ambazo zinafanya baadhi ya upelelezi kuchukua muda mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, iwapo kuna malalamiko dhidi ya Polisi, uchunguzi hufanyika kwa mujibu wa Kanuni ya 103 ya Kanuni za Kudumu za Polisi na Askari akipatikana kwa makusudi akawa na hatia, hatua za kinidhamu na kisheria huchukuliwa dhidi yake.
MHE. FAKHARIA SHOMARI KHAMIS aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa kumekuwa na matukio ya kuvamiwa kwa askari wetu wakiwa katika vituo vyao vya kazi na kujeruhiwa, kunyang„anywa silaha na wakati mwingine hata kuuawa:-
(a) Je, Serikali inatoa tamko gani juu ya usalama wa askari hawa?
(b) Je, mpaka sasa Serikali imeshakamata silaha ngapi zilizoporwa kutoka kwa askari waliovamiwa wakiwa katika majukumu yao?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fakharia Shomari Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) yote kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa usalama wa askari polisi wanapokuwa katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba, Serikali itaendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi hapa nchini kwa vitendea kazi bora na kuwajengea uwezo askari wetu kwa mafunzo ili waweze kukabiliana na matukio ya uhalifu yanayohusisha uvamizi wa vituo vya polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa kipengele cha pili, Jeshi la Polisi limefanikiwa kukamata silaha 19 kati ya 23 zilizoporwa kutoka kwa askari waliovamiwa wakiwa katika majukumu yao katika kipindi cha Julai, 2015 hadi Septemba, 2016.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA aliuliza:-
Mkoa wa Tabora unakabiliwa na tatizo kubwa la msongamano wa mahabusu kiasi cha kutishia afya zao kwa sababu magereza hayo yana uwezo wa kuchukua takribani mahabusu 1200, lakini mpaka sasa kuna zaidi ya mahabusu 2500 kinyume kabisa na haki za mahabusu:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa hali ya magereza katika Mkoa wa Tabora zinaboreshwa na idadi hiyo ya mahabusu inazingatia haki za msingi za binadamu?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kesi zilizopo mahakamani zinaharakishwa kwa kuwa wapo mahabusu wengi ambao wana kesi za kubambikiwa au kughushiwa tu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kwamba hali ya magereza katika Mkoa wa Tabora pamoja na mikoa mingine nchini zinaboreshwa ili kuzingatia haki za binadamu, Serikali inaendelea kufanya upanuzi wa magereza kwenye magereza ya zamani na kujenga magereza mapya ya mahabusu katika kila Wilaya ambapo mpango huu ni endelevu na utekelezaji wake umekuwa ukifanyika kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha wa 2016/2017, Serikali imetenga jumla ya Shilingi bilioni tatu katika bajeti ya fungu la maendeleo kwa ajili ya ukarabati na upanuzi na umaliziaji wa ujenzi wa mabweni mapya na majengo ya utawala katika baadhi ya magereza nchini likiwemo Gereza la Nzega na Gereza la Mahabusu Urambo. Kati ya fedha hizo, milioni 150 ni kwa ajili ya kuanza upanuzi wa gereza la Nzega kwa kujenga mabweni mawili ya wafungwa yenye uwezo wa kuchukua wafungwa 50 kila moja na milioni 35 ni kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa bweni moja la wafungwa ambalo linatarajiwa kujengwa liwe gereza la mahabusu huko Urambo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua kuwa kuna msongamano wa mahabusu katika gereza la Tabora kama ilivyo katika magereza mengine hapa nchini. Kwa kutambua hilo, Serikali kupitia Jukwaa la Haki Jinai imekuwa ikifanya vikao vya kuharakisha kesi ambazo bado upelelezi wake ulikuwa haujakamilika ili kupunguza msongamano magerezani. Aidha, mafunzo yamekuwa yakitolewa kwa askari wapelelezi ili ukamataji wa watuhumiwa uzingatie uzito wa ushaidi wa mhusika kuepusha malalamiko ya kubambikiwa kesi.
MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS (K.n.y MHE. ABDALLAH HAJI
ALI) aliuliza:-
Usafiri wa bodaboda unatoa ajira kwa vijana walio wengi na kurahisisha usafiri, lakini zimekuwa zikisabaisha ajali nyingi mara kwa mara:-
Je, ni watu wangapi wamepoteza maisha na wangapi wamejeruhiwa na ajali za pikipiki kuanzia mwaka 2010 hadi 2017?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu ndugu yangu Abdallah Haji Ali, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, pikipiki za matairi mawili yaani bodaboda na matairi matatu yaani bajaji zilianza kutumika kubeba abiria kuanzia mwaka 2008. Mwaka 2010 Serikali ilipitisha kanuni na masharti ya usafirishaji wa pikipiki pamoja na bajaji. Aidha, katika kipindi hicho hakukua na utaratibu wowote wa kusimamia biashara ya uendeshaji pikipiki pamoja na bajaji zinazobeba watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipindi cha kuanzia Januari, 2010 hadi Februari, 2017 kumekuwa na jumla ya ajali 31,928 zilizosababisha vifo vya watu 6,529 na majeruhi 30,661.
MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:-
Fomu ya PF3 hutolewa na polisi tukio linapotokea na kumletea usumbufu mgonjwa kwani anatakiwa kuwa na uthibitisho wa fomu hiyo ili daktari atoe ushauri wake na pia mgonjwa hawezi kupatiwa huduma yoyote mpaka awe na fomu hiyo hata kama ana maumivu makali au hali yake ni mbaya;
Je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kufanya marekebisho ya utaratibu ili kuwaondolea usumbufu wagonjwa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu mama yangu Mwanne Ismail Mchemba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshmiwa Naibu Spika, Serikali iliweka utaratibu wa mtu anapokuwa ameumia apate Police Form No. 3 kwa mujibu wa Kifungu cha 170 cha Kanuni za Kudumu za Jeshi la Polisi ili aweze kupokelewa na kupewa matibabu katika hospitali zetu. Msingi mkubwa wa hiyo fomu ni kutaka kujua mazingira ya mtu huyo aliumia wapi na alikuwa anafanya nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, PF3 inatumika pia kama kielelezo Mahakamani kama mtu ameshambuliwa ama amepigwa ili Mahakama ijue ameumia kiasi gani na kwa kuwa rahisi kutoa adhabu stahiki. Hata hivyo, kuna matukio mengine yaliyo wazi ambayo PF3 hupelekwa hospitali kwa urahisi wa matibabu na kwa msingi huo PF3 bado inakidhi matakwa yaliyokusudiwa kwa mujibu wa kifungu nilichokitaja hapo juu.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL aliuliza:- Mkoa wa Kilimanjaro una tatizo la uhaba wa magari ya zimamoto; gari linalofanya kazi mpaka sasa ni moja tu, hivyo kufanya huduma ya zimamoto kuwa duni sana.
(a) Je, ni lini Serikali itaongeza magari mengine mawili ili kusaidia shughuli za zimamoto na kuepusha hasara zinazowakabili wananchi wanaopata majanga ya moto?
(b) Je, Serikali haioni kwamba uamuzi wa kuhamishia Kitengo cha Zimamoto Wizara ya Mambo ya Ndani umeiongezea mzigo Wizara hiyo na kupunguza ufanisi wa shughuli za zimamoto?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Raphael Japhary Michael, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Mkoa wa Kilimanjaro una gari moja kubwa la kuzima moto ambalo lina uwezo wa kubeba maji lita 7,000 na dawa za kuzimia moto wa mafuta lita 400.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa sasa kuna magari mawili madogo ya kuzimia moto yasiyo na matanki ya kubeba maji na madawa. Pamoja na magari haya, hufanya kazi kwa kupata maji kutoka gari lingine au kutoka katika vituo maalum vya maji ya kuzimia moto (fire hydrant). Hata hivyo, kwa sasa ni gari moja tu linalofanya kazi na lingine linahitaji matengenezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango wa kununua magari ya zimamoto na uokoaji kwa ajili ya Mkoa wa Kilimanjaro pamoja na mikoa mingine. Katika kutekeleza mpango huo, Serikali inafanya mazungumzo na taasisi mbalimbali za nje ya nchi ambazo zimeonyesha nia ya
kutukopesha fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari ya zimamoto pamoja na uokoaji na mazungumzo yatakapokamilika mkataba utasainiwa na kuanza utekelezaji wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhamishwa kwa Kitengo cha Zimamoto kutoka katika mamlaka mbalimbali na kuwekwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kulifanyika baada ya tathmini hususan ya utendaji kazi za kila siku, ambapo ilibainika kuwa utendaji kazi wa Vikosi vya Zimamoto
katika Halmashauri ulikuwa dhaifu kutokana na vikosi hivyo kuwa chini ya Wahandisi wa Majiji, Manispaa na Miji ambapo hawakuwa na utaalam wa masuala ya Zimamoto na Uokoaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, ilibainika pia kuwa vikosi vikiwa chini ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege vihamishiwe Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ili kuleta ufanisi zaidi wa kazi na viwe chini ya kamandi moja ili viweze kupokea amri kutoka kwa Kamishna Jenerali wa Jeshi la
Zimamoto na Uokoaji. Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba uamuzi huo uliongeza ufanisi na siyo mzigo.
MHE. HAMAD SALIM MAALIM aliuliza:-
Miongoni mwa stahiki za askari polisi anapohamishwa kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine ni nauli ya askari huyo na wategemezi wake pamoja na fedha za kusafirishia mizigo:-
Iwapo mwajiri atashindwa kumlipa askari huyo stahiki
zake zote hizo, je, askari huyo atapaswa kuhama kwa gharama zipi na kuripoti mkoa wake mpya aliopangiwa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamad Salim Maalim, Mbunge wa Kojani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi hutoa uhamisho kulingana na mahitaji pale Inspekta Jenerali wa Polisi anapoona kuna umuhimu wa kuongeza nguvu eneo fulani ambalo ni tete kwa wakati huo. Hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 59(5)(a) ya Kanuni za Jeshi la Polisi (PGO). Askari anayehamishwa atalipwa mafao yake kama ilivyoelekezwa katika Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma, Toleo Na. 259 iwapo hakuhamishwa kwa makosa ya kinidhamu. Aidha, askari anayeomba kuhama eneo moja kwenda eneo lingine kwa sababu zake binafsi hatalipwa mafao hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia maelezo hayo, inapotokea dharura ya askari kuhitajika kwenda kutoa huduma eneo lingine, askari husika atatekeleza amri ya uhamisho haraka wakati stahili zake zinafanyiwa kazi kwa mujibu wa taratibu za fedha. Kwa taratibu za Kijeshi, askari hawezi kusubiri malipo katika mazingira ambayo anakwenda kuokoa maisha ama kulinda maslahi ya Taifa katika eneo husika.
MHE. ORAN M. NJEZA (K.n.y. MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE) aliuliza:-
Hivi karibuni kumetokea mapigano baina ya wakulima na wafugaji ambayo yamesababisha baadhi ya Watanzania kupoteza maisha na wengine kupata ulemavu wa maisha:-
Je, Serikali imejipangaje kupambana na janga hilo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwa na migogoro kati ya wakulima na wafugaji katika maeneo kadhaa ndani ya nchi yetu ambayo yamesababisha Watanzania kupoteza maisha na wengine kupata ulemavu wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na hali hiyo Serikali kupitia Jeshi la Polisi inaendelea kushauriana na Mamlaka zinasosimamia matumizi bora ya ardhi, kutenga maeneo yatakayotumiwa na wakulima na wafugaji ili kuepusha migogoro na kutoa elimu kwa wakulima na wafugaji juu ya mazingira bora ya matumizi ya ardhi. Aidha, Jeshi la Polisi hufanya doria na misako na kukamata wale wanaovunja Sheria punde panapokuwepo na mwingiliano wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yanayosababisha migogoro.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO (K.n.y. MHE. NAJMA MURTAZA GIGA) aliuliza:-
Matumizi ya SHISHA yamegundulika kuwa ni miongoni mwa aina ya uvutaji wa sigara ambao wauzaji wengine huchanganya na aina mbalimbali za dawa za kulevya na vileo vikali na kusababisha vijana wadogo kuathiriwa kwa kiasi kikubwa.
Je, kwa nini Serikali hadi sasa inaendelea kuruhusu matumizi ya SHISHA kwenye baadhi ya migahawa na hoteli kubwa ambayo inatumiwa na watu wa rika zote?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Najma Giga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali mara baada ya kuona kuwa matumizi ya shisha yanaleta athari kubwa kwa afya za binadamu, kutokana na utafiti uliofanywa na Wizara ya Afya, Serikali ina mpango mkakati wa kutengeneza utaratibu wa kudhibiti na kutungia sheria kupiga marufuku utumiaji, uuzwaji na usafirishwaji wa shisha nchini Tanzania ili kuweza kuokoa afya za Watanzania walio wengi ambao ni nguvu kazi ya Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tukiwa tunasubiri kutungwa kwa sheria na kanuni, Mheshimiwa Waziri Mkuu alishaelekeza kupiga marufuku matumizi ya shisha na utekelezaji ulishaanza kutekelezwa mikoani ikiwemo Dar es Salaam, Mbeya, Mwanza, Kilimanjaro na mikoa mingine.
MHE. HAMIDU H. BOBALI aliuliza:-
Gereza la Kingulungundwa lililopo Wilayani Lindi linakabiliwa na uhaba mkubwa wa Nyumba za Askari na miundombinu mibovu:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha makazi ya Askari katika Gereza hilo?
(b) Gereza hili lipo umbali wa kilometa tatu kutoka barabara kuu inayotoka Dar es Salaam kwenda Lindi, lakini wakati wa masika, barabara hiyo haipitiki kwa gari kutokana na kujaa tope na maji. Je, Serikali haioni kuwa kukosekana kwa mawasiliano ya barabara kutoka Gerezani ni jambo la hatari?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamidu Bobali, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inafahamu kuwa lipo tatizo la uchakavu na upungufu wa nyumba za Askari wa Jeshi la Magereza nchini na hali hiyo inatokana na baadhi ya nyumba kujengwa kabla ya uhuru ama katika maeneo mengine ambapo zilijengwa kwa matumizi ya muda wakati ikisubiri ujenzi wa nyumba za kudumu na za kisasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya nyumba za Askari Magereza hivi sasa ni nyumba 14,500 wakati zilizopo ni nyumba 4,221, hivyo kuwepo kwa upungufu wa nyumba 10,279 ambao unasababisha baadhi ya Askari kuishi nje ya Kambi. Kwa sasa Serikali ina mpango wa kuwajengea Askari Magereza nyumba 9,500 na mara baada ya mpango huo kukamilika tunategemea kumaliza kero za makazi ya Askari Magereza nchini likiwemo Gereza alilolitaja Mheshimiwa Mbunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo hilo, Serikali imeendelea na mpango wa kuzifanyia ukarabati mkubwa baadhi ya nyumba kwenye baadhi ya Magereza na kujenga nyumba mpya. Ni nia ya dhati ya Serikali kuendelea kuboresha nyumba za Askari nchini zikiwemo za Gereza la Kingulungundwa kwa awamu. Kwa sasa, Jeshi la Magereza linajenga nyumba 320 za Maafisa na Askari hapo Ukonga na fedha ambayo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameshatoa ni shilingi bilioni 10 na shilingi bilioni tano tayari zilishatolewa kwa ajili ya ujenzi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara inayotoka barabara kuu ya Dar es Salaam kuelekea Gereza la Kingurungundwa imekuwa haipitiki kwa gari wakati wa masika. Kimsingi barabara hiyo ipo chini ya Halmashauri ya Wilaya ya Lindi vijijini na ndiyo yenye jukumu la kuifanyia matengenezo barabara hiyo kwa kuwa haiishii Gerezani tu, bali inaendelea kwenye vijiji vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza limeshafanya mawasiliano na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lindi Vijini ili barabara hiyo iweze kutengenezwa na kuepusha adha inayojitokeza wakati wa masika.
MHE. DEVOTHA M. MINJA (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-
Magereza mengi nchini hayapo katika viwango na ubora unaotakiwa na hivyo kuvunja haki za wafungwa.
Je, Serikali ina mkakati gani katika kufanya matengenezo na kulinda haki za wafungwa?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Magereza limekuwa likitekeleza na kusimamia haki za wafungwa magerezani kwa kuzingatia Sheria ya Magereza Na. 34 ya mwaka 1967 (The Prisons Act. No. 34 of 1967 CAP. 58 R.E 2002) pamoja na sheria nyingine na Kanuni za Uendeshaji wa Magereza za mwaka 1968 (The Prisons (Prison Management) Regulations of 1968) G.N.19 of 23/01/1968 na marekebisho yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, haki za wafungwa zinazotekelezwa na kusimamiwa magerezani kwa mujibu wa Sheria ya Magereza na Kanuni zake nilizozitaja au msingi mwingine, chimbuko lake ni Mkataba wa Kimataifa unaohusu Taratibu na Haki za Wafungwa na Mahabusu. Haki hizo zimeainishwa wazi sehemu ya VII na IX ya Sheria ya Magereza na Kanuni za Uendeshaji wa Magereza kama ifuatavyo:-
(i) Haki ya kutenganishwa ambapo wafungwa hutenganishwa kutokana na umri wao, jinsia, aina ya kosa, afya na tabia.
(ii) Haki ya kupatiwa chakula na mahitaji mengine. Mfungwa hupewa chakula kama ilivyoainishwa na Kanuni za Uendeshaji wa Magereza niliyoitaja.
(iii) Haki ya kuwa na uhuru wa kupata mawasiliano na kutembelewa na ndugu na jamaa zake. Mawasiliano haya ni pamoja na kupokea na kuandika barua, kusoma magazeti na kusikiliza taarifa mbalimbali kutoka katika vyombo vya habari.
(iv) Huduma za afya. Huduma hizi hutolewa kwa mfungwa pindi anapoumwa wakati wote awapo gerezani.
(v) Haki ya kupatiwa malazi safi na ya kutosha ambapo mfungwa mmoja anahitaji eneo la mita za mraba 2.8.
(vi) Haki ya kukata rufaa pale anapoona hakutendewa haki katika hukumu iliyotolewa na Mahakama dhidi yake.
(vii) Haki ya kucheza michezo. Mfungwa anayo haki ya kushiriki na kucheza michezo ya aina mbalimbali na hii inafanyika magerezani.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, zipo changamoto kwa Jeshi la Magereza zinazojitokeza katika kutekeleza baadhi ya haki hizo kutokana na msongamano wa wafungwa katika baadhi ya magereza na kutokana na hali halisi katika baadhi ya maeneo hayo niliyoyataja.(Makofi)
MHE. USSI SALUM PONDEZA aliuliza:-
Askari Polisi Zanzibar kwa muda mrefu wamekuwa wakilazimika kutumia fedha zao za mfukoni kuwahudumia chakula mahabusu wanoshikiliwa katika Vituo vya Polisi Unguja wakati jukumu hilo ni la Serikali.
(a) Je, Serikali imechukua hatua gani za kuondoa tatizo hilo tangu kulalamikiwa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora baada ya kufanya ziara ya ukaguzi na kugundua tatizo hilo?
(b) Je, ni sababu gani zimepelekea chakula kutopelekwa katika Vituo vya Polisi wakati Bunge limekuwa likiridhia matumizi ya Wizara kila mwaka zikiwemo gharama za chakula kwa mahabusu?
(c) Je, haki za binadamu zinazingatiwa vipi inapotokea askari hawana fedha za kununua chakula cha mahabusu na kulazimika kulala na njaa wakati Serikali ndiyo yenye jukumu la kuwapatia huduma ya chakula?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ussi Pondeza, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, mahabusu wanaoshikiliwa katika Vituo ya Polisi huhudumiwa na Jeshi la Polisi kwa kuwapatia mahitaji muhimu kama chakula na malazi. Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikitenga bajeti kwa ajili ya chakula cha mahabusu kwa kila mwaka.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, si kweli kwamba chakula huwa hakipelekwi katika mahabusu za polisi. Chakula hupelekwa kulingana na idadi ya mahabusu kama ambavyo taratibu za utoaji wa chakula zinavyoelekeza katika PGO 356.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, kulisha mahabusu walioko katika Vituo ya Polisi ni jukumu la Serikali na si askari mmoja mmoja kutumia fedha zake za mfukoni kwa kufanya jukumu hilo. Serikali itaendelea kutimiza wajibu huo na hakuna uvunjaji wa haki za binadamu katika kuwapatia huduma za chakula mahabusu.
MHE. MOHAMMED JUMA KHATIB aliuliza:-
Kumezuka wimbi kubwa sana lenye kutisha la ajali za bodaboda nchini kiasi cha kufanya hospitali zetu kupungukiwa na uwezo wa kuwahudumia waathirika wote wa ajali hizo.
(a) Je, Serikali inaweza kulieleza Taifa sababu za kutokea kwa wingi kwa ajali hizo?
(b) Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na utitiri wa ajali hizo bila kuathiri ajira hiyo ya bodaboda?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Mohammed Juma Khatib, Mbunge wa Chonga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, pikipiki za matairi mawili (Bodaboda) na za matatu (Bajaj) zilianza kutumika kubeba abiria mwaka 2008 Tanzania Bara na mwaka 2009 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania liliridhia vyombo hivyo vitumike kutoa huduma ya usafirishaji wa abiria. Sababu kubwa za kutokea kwa ajali zinazohusisha bodaboda na bajaj ni uzembe wa baadhi ya waendesha pikipiki na bajaji kutokufuata Sheria na Kanuni za Usalama Barabarani kwa kiwango kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimekuwa nikijibu hapa Bungeni, Serikali inatambua biashara hiyo inayofanywa na pikipiki za kubeba abiria na inathamini mchango huo katika kutoa ajira katika mikoa yote ya Tanzania Bara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na ajali nyingi zinazosababishwa na bodaboda, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua dhidi ya waendesha pikipiki ambao hawazingatii Sheria ya Usalama Barabarani na kanuni zake pamoja na masharti ya leseni za usafirishaji. Aidha, Jeshi la Polisi limekuwa likitoa mafunzo kwa waendesha bodaboda juu ya matumizi bora ya barabara.
MHE. ASHA MSHIMBA JECHA aliuliza:-
Kituo cha Polisi Dunga kimechakaa sana kwani kuta zake zimepasuka na baadhi ya vyumba havitumiki kutokana na kuhatarisha usalama wa askari na wananchi wanaofika kwa ajili ya kupata huduma. Je, ni lini Serikali itajenga upya kituo hicho?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Mshimba Jecha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Kituo cha Polisi Dunga pamoja na Wilaya zote mpya zilizoanzishwa katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Kwa kutambua umuhimu wa Kituo cha Polisi Dunga, tathmini itafanyika ili gharama halisi ziweze kujulikana. Aidha, ujenzi wa kituo hicho utaanza mara baada ya fedha kupatikana kwa ajili ya kipaumbele cha Serikali na hivi sasa katika kukamilisha miradi ya zamani ya polisi na kuanza miradi mipya ya ujenzi wa vituo hivyo vya polisi.
Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali kuimarisha miundombinu ya ulinzi na usalama, tunatoa wito kwa wadau mbalimbali wa maendeleo kushiriki katika ujenzi wa vituo vya polisi ili huduma za ulinzi na usalma ziweze kupatikana kwa karibu.
MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatenga bajeti kwa ajili ya kuwajengea nyumba askari polisi wa Pemba ili kuwaondolea adha ya makazi askari hao?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI aliuliza:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa nyumba za kuishi askari Pemba hazitoshi kama ilivyo katika maeneo mengine nchini na hivyo kusababisha adha kwa askari wetu. Serikali itatenga bajeti katika mwaka ujao wa fedha ili kujenga nyumba za askari wa Zanzibar husasan Pemba ambako Mheshimiwa Mbunge ameuliza ili kuwaondolea adha wanazozipata kutokana na kutokuwa na nyumba za kutosha. (Makofi)
MHE. ZUBEDA H. SAKURU aliuliza:- Hivi sasa kumekuwa na wimbi la matukio ya ukamataji wa Wahamiaji haramu kwa wingi hapa nchini. Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya ongezeko la matukio hayo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Idara ya Uhamiaji imekuwa ikiendelea na mapambano dhidi ya wahamiaji haramu na kuwachukulia hatua za kisheria ili kuhakikisha nchi yetu inakuwa salama. Katika kupambana na wahamiaji haramu Idara ya Uhamiaji huchukua hatua zifuatazo:-
(i) Kuendesha doria za misako ya mara kwa mara katika maeneo mbalimbali nchini kwa kushirikiani na vyombo vya Ulinzi na Usalama ambapo katika mwaka 2016/2017 jumla ya watuhumiwa 9.581 na wahamiaji haramu walikamatwa na kuchukuliwa hatua mbalimbali kisheria.
(ii) Serikali inaendelea kuimarisha vitendea kazi kama vile magari na kupanua wigo wa watumishi ili kuweza kudhibiti mipaka mingi iliyopo na kutoa elimu kwa umma juu ya madhara ya kuhifadhi wahamiaji haramu na kupambana na mitandao wa wasafirishaji haramu wa binadamu.
Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali ni kuendelea kuimarisha ulinzi wa mipaka na Serikali inaagiza wageni wote wanaoingia nchini wafuate sheria za nchi na wale ambao hawatafuata sheria hizo watachukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na wale wanaojihusisha na usafirishaji na wale wanaowaficha wahamiaji haramu kuacha tabia hizo kwa sababu Serikali itachukua hatua kali punde itakapojiridhisha kwamba kuna watu wamefanya vitendo hivyo.
MHE. KASUKU S. BILAGO aliuliza:-
Jimbo la Buyungu Wilayani Kakonko linapakana na nchi ya Burundi, hivyo raia wa nchi hizi mbili wanafanya baadhi ya shughuli za kibiashara na kijamii kwa kushirikiana kwa muda mrefu hata kabla ya Burundi kujiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
(a) Je, ni lini Serikali itafungua Ofisi ya Uhamiaji katika kijiji cha Muhange iliyofungwa bila sababu za msingi?
(b) Je, kwa nini Warundi wakija kufanya biashara kwenye masoko ya ujirani mwema au kulima mashamba hukamatwa na kufungwa jela?
(c) Je, kwa nini Warundi 254 waliofungwa kwa makosa kama hayo wasirudishwe kwao ili kupunguza msongamano magerezani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kasuku Samson Bilago, Mbunge wa Buyungu, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Uhamiaji katika Kijiji cha Muhange ilifungwa kutokana na sababu za kiusalama baada ya nchi jirani ya Burundi kuingia katika machafuko miaka ya 1990. Hata hivyo Serikali itaangalia endapo mazingira ya sasa yanaruhusu kujenga Ofisi hiyo.
(b) Mheshimiwa Spika, Idara ya Uhamiaji inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria na taratibu zinazoruhusu wageni kuingia nchini, kuishi na kufanya kazi. Hivyo, wageni wote waingiapo nchini wakiwemo raia wa Burundi wanapaswa kuafuata sheria na taratibu zilizopo.
(c) Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna msongamamno wa wafungwa katika Magereza yetu nchini kutokana na sababu mbalimbali ambapo kwa sasa kuna jumla ya wafungwa 725, raia wa Burundi katika Mkoa wa Kigoma ambao wamefungwa kwa makosa mbalimbali.
Hata hivyo, ipo sheria inayoruhusu kumrudisha mfungwa kwao kwa yule ambaye sio Mtanzania. Sheria hiyo inaitwa The Transfer of Prisoners Act (No. 10) of 2004 na Kanuni zake (The Transfer of Prisoners Regulations of 2004).
Mheshimiwa Spika, sheria hii inatumika pale tu mfungwa wa nchi nyingine anapoomba kumalizia sehemu kifungo chake kwenye nchi yake ya asili.
MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-
Kuna mjenzi aliyejenga Vituo vya Polisi kupitia Kampuni iitwayo Al Batna Building Co. Ltd. Vituo alivyojenga ni Kituo cha Polisi Mkokotoni - Unguja na Kituo cha Polisi cha Madungu kilichoko Chakechake Pemba kwa gharama ya shilingi 223,440,000.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kulipa deni hilo tangu 2012 hadi leo hii?
(b) Je, Serikali inayo taarifa kwamba mwenye kampuni hiyo aliyejenga vituo hivyo amepata maradhi makubwa huku akihangaika kufuatilia haki yake hiyo bila mafanikio?
(c) Je, ni lini Serikali itamtembelea na kumpa pole kwa maradhi hayo mabaya yaliyompata?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashimu Ayoub, kama ifuatavyo:-
(i) Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi aliyejenga Kituo cha Polisi Mkokotoni kupitia Kampuni ya Al Batna Building Co. Ltd. alishalipwa shilingi za Kitanzania 560,000,000 na anadai shilingi za Kitanzania 525,000,000 ili kumalizia ujenzi katika kituo hicho. Deni hilo limehakikiwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani na atalipwa mara fedha zitakapokuwa zimetolewa.
(ii) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Serikali nitoe pole kwa mkandarasi wetu kwa maradhi yaliyompata na nimhakikishie kuwa deni lake atalipwa na Serikali iliamua kusitisha malipo kwa Wazabuni wote katika kipindi fulani kwa ajili ya kufanya uhakiki ili kuepuka kulipa madeni mara mbili.
(iii) Mheshimiwa Mwenyekiti, tutamtembelea kumpa pole baada ya kumalizika kwa Mkutano huu wa Bunge lako Tukufu kwa kadri ya upatikanaji wa nafasi.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Kwa kuwa lengo la Serikali kuruhusu vyombo vya usafiri wa pikipiki kubeba abiria na mizigo ni kusaidia kurahisisha usafiri na pia kutoa ajira kwa vijana hapa nchini lakini ajali zinazotokana na vyombo hivi kwa sasa ni nyingi kuliko vyombo vingine.
(a) Je, Serikali inaweza kueleza ni ajali ngapi za bodaboda zimetokea kwa miaka mitatu toka mwaka 2015
- 2017 na ni watu wangapi wamepoteza maisha kwenye ajali hizo na walemavu ni wangapi?
(b) Je, Serikali ina mikakati gani ya uhakika ya kuokoa maisha na nguvukazi ya Taifa inayopotea kwa usafiri huu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Magdalena Sakaya, Mbunge wa Kaliua, kama ifuatavyo:-
(i) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitatu toka Januari, 2015 hadi Februari, 2017 jumla ya ajali 5,418 za bodaboda zilitokea na kusababisha vifo vya watu 1,945 na majeruhi 4,696.
(ii) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi inayo mikakati ya kukokoa maisha na nguvu kazi ya Taifa inayopotea kutokana na ajali za bodaboda. Mikakati hiyo ni pamoja na:-
(a) Kupitishwa kwa Kanuni ya Leseni za Pikipiki na Bajaji iliyopita mwaka 2009;
(b) kutoa elimu ya Usalama Barabarani mashuleni na kupitia vipindi vya redio, televisheni pamoja na vipeperushi;
(c) Kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa waendesha bodaboda;
(d) Kuimarisha usimamizi wa Sheria za Barabarani;
(e) Kusisitiza madereva wa bodaboda kuepuka kuendesha kwa mwendo kasi;
(f) Kuchukua hatua kwa vitendo vyote vya ulevi na kuweka viakisi mwanga (reflectors) ili kuonekana kwa urahisi; na
(g) Kusisitiza matumizi ya kofia ngumu ili kupunguza madhara punde ajali zinapojitokeza.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL aliuliza:-
Gereza la Karanga ni chakavu na lina uhaba wa samani:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kulikarabati gereza hilo?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha za kutosha za uendeshaji ili kununua samani pamoja na vifaa vingine vitakavyosaidia kutoa huduma kwa wafungwa na mahabusu gerezani hapo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raphael Japhary Michael, Mbunge wa Moshi Vijijini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
– Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba Gereza la Karanga linakabiliwa na uchakavu wa miundombinu na hali hiyo imetokana na majengo na miundombinu ya gereza hilo kuwa ya tangu mwaka 1949 likiwa na uwezo wa kuhifadhi wahalifu 814 na wahalifu waliopo sasa ni takriban 1,200. Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali inatekeleza mpango wa muda mrefu wa kuyaboresha majengo hayo kwa kuyafanyia ukarabati mkubwa unaolenga kuyaimarisha na kuyaboresha pamoja na kuyafanyia upanuzi.
– Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa na mpango wa kupeleka fedha za maendeleo kwa ajili ya ukarabati na ununuzi wa samani katika magereza yote nchini likiwemo Gereza la Karanga. Aidha, kutokana na ufinyu wa bajeti, fedha hizo zimekuwa zikitolewa kwa awamu katika magereza mbalimbali nchini.
MHE. DOTO M. BITEKO aliuliza:-
Askari wa Wilaya ya Bukombe wanazo changamoto nyingi zikiwemo ukosefu wa nyumba za askari.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia nyumba askari hao katika Wilaya ya Bukombe?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu Sali la Mheshimiwa Doto Mashaka Biteko, Mbunge wa Bukombe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli Jeshi la Polisi lina changamoto mbalimbali ikiwemo uchache wa nyumba za kuishi askari. Wilaya ya Bukombe ambayo ina jumla ya maafisa wakaguzi na askari 122 ni miongoni mwa Wilaya zenye changamoto za uhaba wa nyumba za kuishi askari.
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga nyumba za kuishi askari katika mikao ya wialaya kwa awamu. Katika Wilaya ya Bukombe, Jeshi la Polisi lipo kwenye mazungumzo na Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe ili kupatiwa eneo kwa ajili ya kujenga nyumba za kuishi askari. Baada ya kupatiwa eneo hilo Serikali itajenga nyumba hizo kwa fedha za bajeti kwa kadri fedha zitakavyopatikana kwa jinsi ilivyotengwa pamoja na kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo.
MHE. SILAFU J. MAUFI
Serikali imerejesha mafunzo ya JKT nchini. Je, ni lini Kambi ya JKT ya Luwa Mkoani Rukwa itafufuliwa ili kuandaa vijana wetu?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silafu Maufi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi ya Luwa JKT ilifufukiwa na sasa kimekuwa Kikosi na kimepewa namba 846 Kikosi cha Jeshi yaani 846 KJ kuanzia tarehe 01 Desemba, 2016.
Aidha, vikosi vilivyoanzishwa sambamba na kikosi hicho ni pamoja na Kikosi cha Jeshi 826 kilichopo Mpwapwa hapa Dodoma, 839 Kikosi cha Jeshi kilichopo Makuyuni, Mjini Arusha, 845 Kikosi cha Jeshi kilichopo Itaka, Mkoani Songwe na 847 Kikosi cha Jesi kilichopo Milundikwa, Mkoani Rukwa.
MHE. NURU A. BAFADHILI aliuliza:-
Askari Polisi wengi katika Jiji la Tanga wanaishi uraiani ambapo ni kinyume cha maadili kutokana na ukosefu wa nyumba za kuishi katika kambi zao.
• Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga upya nyumba za askari hao?
• Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwajengea nyumba za ghorofa askari wa Kambi za Chumbageni, Mabawa na Madina Msambweni, ili ziweze kuwaweka askari wengi katika eneo moja, kama ilivyo Kilwa Road Dar es Salaam?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nuru Awadh Bafadhili, Mbunge wa Viti Maalum, lenye kipengele (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uchakavu wa nyumba za kuishi askari katika Jiji la Tanga na maeneo mengine hapa nchini. Katika kukabiliana na tatizo la uchakavu na upungufu wa nyumba za kuishi askari polisi, Serikali ina mpango wa kujenga nyumba mpya katika Jiji la Tanga na maeneo mengine kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona umuhimu wa kujenga nyumba za ghorofa kwa ajili ya makazi ya askari, kama ilivyojenga nyumba za Kilwa Road Jijini Dar es Salaam, Ziwani kwa upande wa Zanzibar pamoja na Buyekela Mwanza kwa kuwa zina uwezo wa kuchukua familia nyingi katika eneo dogo la ardhi. Aidha, taratibu za ujenzi wa nyumba za kuishi askari polisi Jijini Tanga zitakapoanza wataalam watazingatia ushauri wa Mheshimiwa Mbunge.
MHE. USSI SALUM PONDEZA (K.n.y. MHE. JAFFAR SANYA JUSSA) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itavipatia Vituo vya Polisi vya Paje na Jambiani samani za ofisi pamoja na magari kwa ajili ya patrol?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaffar Jussa, Mbunge wa Paje, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna uhaba wa magari pamoja na samani katika Vituo vya Polisi vya Paje na Jambiani, kama ilivyo kwenye maeneo mengine hapa nchini. Kwa sasa Vituo vya Polisi cha Paje na Jambiani vinapata huduma za doria kutoka kwa OCD wa Makunduchi, hali inayosababisha kuwa na changamoto katika utekelezaji wa majukumu ya kiusalama.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi lipo katika mchakato wa kupokea magari mapya yaliyonunuliwa na Serikali ambayo yatagawawiwa kwa kuzingatia kiwango cha uhalifu, idadi ya watu na ukubwa wa eneo katika kamandi husika. Aidha, Jeshi la Polisi litaendelea kutumia bajeti inayotengwa kutimiza azma ya Serikali ya kuhakikisha kuwa linakuwa na vitendea kazi vya kutosha, ikiwa ni pamoja na magari na samani katika vituo vya Polisi kote nchini.
MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:-
Kumekuwa na idadi kubwa ya ajali nchini zinazosababisha vifo, majeruhi na upotevu wa mali:-
• Je, kwa kipindi cha miaka miwili kuanzia 2016
– 2018 ni ajali ngapi zimetokea na kusababisha vifo au majeruhi?
• Je, ni waathirika wangapi waliomba fidia na wangapi mpaka sasa wamelipwa fidia zao kutoka kampuni za bima?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Tweve, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa katika kipindi cha mwaka 2016 hadi 2018 Jeshi la Polisi kupitia Kikosi cha Usalama Barabarani lilichukua hatua za makusudi kupunguza ajali ambapo mpaka kufikia Disemba, 2017 limefanikiwa kupunguza ajali za barabarani kwa asilimia 43.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 kulitokea jumla ya ajali 9,856 ambazo zilisababisha vifo 3,256 na majeruhi 2,128. Mwaka 2017 kulitokea ajali 5,310 ambazo zilisababisha vifo 2,533 na majeruhi 5,355 wakati kwa kipindi cha Januari hadi Februari, 2018 zimetokea ajali 769 ambazo zimesababisha vifo 334 na majeruhi 698.
• Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2016 hadi 2018 jumla ya waathirika wa ajali 1,583 walilipwa fidia yenye jumla ya thamani ya fedha za kitanzania bilioni 7.3 kutoka kampuni mbalimbali za bima.
MHE. DKT. SULEIMAN ALLY YUSSUF aliuliza:-
Kuna ushahidi wa kutosha kwamba kuna watu kadhaa ambao wamekuwa wakikamatwa na Jeshi la Polisi Unguja na Pemba huku baadhi yao wakifunguliwa mashtaka na wengine kuachiwa:-
(a) Je, ni kwa nini Jeshi la Polisi linashindwa kufanya kazi kwa weledi na kukamata watu pasipo ushahidi kwa lengo la kukomoa tu?
(b) Ili kulisafisha Jeshi la Polisi, je, Serikali haioni haja ya kuwawajibisha watendaji ambao wenye tabia ya kuwakomoa wananchi kwa kuwakamata pasipo ushahidi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Dkt. Suleiman Ally Yussuf, Mbunge wa Mgogoni, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi ni chombo kilichoundwa kwa mujibu wa Katiba na Sheria na linatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba na Sheria na kanuni na taratibu zilizopo, jukumu lake kuu likiwa ni kulinda usalama wa raia na mali zao. Jeshi la Polisi limepewa mamlaka ya kisheria ya kukamata, kuhoji na kuweka watuhumiwa mahabusu kwa muda ulioruhusiwa kisheria endapo itabainika kuwa kuna viashiria au taarifa ya kuhusika katika kutenda kosa la jinai.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa sheria na kanuni na taratibu za utendaji zinazoongoza Jeshi la Polisi linapobainika askari amebambika kesi kwa sababu zozote zile huchukuliwa hatua mbalimbali za kinidhamu ikiwamo kufukuzwa kazi.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA alijibu:-
Kumekuwa na wimbi kubwa la uhalifu unaofanywa na baadhi ya madereva wa bodaboda na bajaji katika maeneo mengi Jijini Dar es Salaam.
(a) Je, Serikali mpaka sasa imechukua hatua gani kudhibiti wimbi hili linalokuwa tishio kwa watumiaji wa vyombo vya usafiri?
(b) Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuhakiki na kutambua mmiliki, dereva na mahali zinapopaki bajaji na bodaboda?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwepo na ongezeko la uhalifu unaofanywa na waendesha bodaboda ama bajaji katika maeneo mengi Jijini Dar es salaam. Hata hivyo, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kama kufanya doria za magari, doria za pikipiki na za watembea kwa miguu lakini pia kuanzisha na kushirikiana na vikosi vya ulinzi shirikishi ili kubaini na kuzuia uhalifu katika maeneo ya makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Serikali za Mitaa, Halmashauri na Jiji la Dar es Salaam imeendelea kuhakiki pikipiki hizo ikiwa ni pamoja na kuwapangia maeneo ya kuegesha (ku-park). Aidha, kupitia usajili wa TRA na Serikali za Mitaa, Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam imeendelea kuhakiki pikipiki hizo ikiwa ni pamoja na kuanzisha utaratibu wa kuzisajili katika maeneo ya maegesho ili kupata kumbukumbu za mmiliki, dereva na eneo maalum wanaloegesha pikipiki hizo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatatua au kumaliza kabisa tatizo la baadhi ya wakazi wanaoitwa Wahamiaji katika Vijiji vya Nyabuzume, Tiring’ati, Nyaburundi na Bigegu ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakisumbuliwa na hoja hiyo bila kupewa ufumbuzi?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama inavyofahamika nchi yetu, hususan maeneo ya mipakani, imekuwa na tatizo la wahamiaji ambao hufahamika kama walowezi walioingia na kuishi nchini kwa miaka mingi. Wahamiaj hawa waliingia nchini kwa sababu mbalimbali tangu wakati wa ukoloni, ikiwemo kufanya kazi katika mashamba na migodi ya wakoloni, vita vya kikabila na uhaba wa ardhi katika nchi zao na pia kuvutiwa na hali ya amani iliyopo katika nchi yetu. Kwa mujibu wa Sheria ya Uraia, Sura Namba 357, kama ilivyorejewa mwaka 2002 walowezi hawa hawatambuliwi kama raia wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji alivyovitaja Mheshimiwa Mbunge ni miongoni mwa maeneo yenye tatizo hili. Hivyo, kwa kutambua changamoto za tatizo hili Serikali kupitia Idara ya Uhamiaji mwaka 2009 ilifanya sensa ya wahamiaji hao katika maeneo mbalimbali hapa nchini, ikiwa ni pamoja na vijiji tajwa ambapo, ilibaini kijiji cha Nyabuzume kuna walowezi 160, Tiring’ati 48, Nyaburundi 530 na Bigegu 72.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya sensa hiyo, Serikali imekuwa ikiwapatia wahamiaji hao vibali vya kuishi nchini baada ya kukidhi vigezo ili kuwatambua na kuhalalisha ukaazi wao.
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na ada ya Zimamoto ambayo wanatozwa wafanyabiashara katika Halmashauri ya Mji wa Tunduru huku kukiwa hakuna Jeshi la Zimamoto na Uokoaji eneo hilo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Frank Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ada zinazotozwa na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ni kwa mujibu wa Sheria Na. 14 ya 2007 ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Kanuni za Ukaguzi za mwaka 2008 na Marekebisho yake ya mwaka 2012 na 2014. Sheria na Kanuni hizi zinamtaka mmiliki wa chombo cha usafiri pamoja na usafirishaji, mmiliki wa jengo refu au fupi, chombo cha usafiri na usafirishaji, mfanyabiashara au ofisi kulipia tozo ya ukaguzi. Tozo hizo zimepangwa kutokana na ukubwa wa jengo na hatari ya moto kwenye eneo husika.
Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Momba Mkoani Songwe, Halmashauri ya Tunduma ina kituo cha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ambacho kipo katika Mtaa wa Kilimanjaro na kina askari kumi na gari moja la kuzimia moto. Kwa sasa gari hilo lipo Jijini Mbeya kwa ajili ya matengenezo. Wizara kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji inafanya jitihada za haraka ili gari hilo litengamae na kurejea kituoni.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, askari wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji wanaendelea na majukumu yao mengine ya kutoa elimu ya kinga na tahadhari za moto na ukaguzi wa majengo ili kuzuia ajali za moto na majanga mengine. (Makofi)
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA aliuliza:-
(a) Je, ni lini Serikali itawapatia gari lingine Kituo cha Polisi Magharibi ‘A’ ili kupunguza matumizi ya magari binafsi kwa Jeshi la Polisi?
(b) Je, Serikali imejipanga vipi kupunguza uhalifu unaojitokeza mara kwa mara?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Bububu lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la upungufu wa vitendea kazi katika Jeshi la Polisi hususan magari ya doria kote nchini ikiwemo Bububu. Kwa kuzingatia umuhimu wa doria katika kudhibiti masuala ya usalama wa raia, Serikali inaendelea kuongeza idadi ya magari na vitendea kazi vinginevyo kadiri hali ya uchumi inavyoruhusu. Mpango ya Jeshi la Polisi ni kupeleka gari moja katika Wilaya ya Magharibi ‘A’ mara baada ya kupokea magari mapya katika siku za hivi karibuni.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi imeendelea kutekeleza jukumu lake la msingi la ulinzi wa raia pamoja na mali zao ili kuhakikisha wananchi na mali zao wanakuwa katika hali ya usalama. Katika kutekeleza jukumu hilo ipo mikakati mbalimbali ambayo imetekelezwa ikiwa ni pamoja na kufanya doria na operesheni za mara kwa mara, kutoa elimu kwa jamii ili kuwajengea uwezo wa kutambua matendo yanayoashiria uhalifu na kutoa taarifa polisi kwa lengo la kuchukua hatua kabla uharibifu kufanyika. (Makofi)
MHE. SULEIMAN A. SADDIQ (K.n.y. MHE. IBRAHIM HASSANALI RAZA) aliuliza:-
Kituo cha Polisi Mazizini kilichopo Kiembe Samaki kipo katika hali mbaya na hakina vitendea kazi, jengo ni chakavu, hakina gari na mazingira yake hayaridhishi:-
Je, ni lini Serikali itaboresha kituo hicho kwa kutatua changamoto zilizopo?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ibrahim Hassanali Raza, Mbunge wa Kiembe Samaki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hali na mazingira ya Kituo cha Polisi Mazizini hairidhishi kutokana na uchakavu wa jengo pamoja na uhaba wa vitendea kazi kama ilivyo kwa baadhi ya vituo katika maeneo mbalimbali. Kituo cha Polisi Mazizini kina majengo mawili. Katika mwaka 2015 Serikali ilifanya ukarabati wa jengo moja la kituo hiki ambapo ukarabati ulikamilika na tayari jengo hilo linatumika kwa kutoa huduma kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, Jeshi la Polisi limependekeza kwa ajili ya maendeleo ya vituo kiasi cha shilingi bilioni 3.7 kwa ajili ya ukarabati na kuboresha miundombinu mbalimbali ya Jeshi la Polisi kote nchini ikiwemo ukarabati wa jengo la pili la Kituo cha Polisi Mazizini Jimboni Kiembe Samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kufanya ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya Jeshi la Polisi na kuongeza vitendea kazi kama vile magari awamu kwa awamu ili kutatua changamoto zinazokabili Jeshi la Polisi katika maeneo mbalimbali.
MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO (K.n.y. MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO) aliuliza:-
Kuna upungufu wa magari katika Vituo vya Polisi Mkoa wa Ruvuma. Yaliyopo sasa ni mabovu kabisa na hayafanyiwi matengenezo kutokana na ukosefu wa fedha.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka magari kwenye vituo hivyo?
(b) Je, ni lini Serikali itapeleka pesa kwenye vituo hivyo kwa ajili ya matengenezo ya magari na mafuta ya magari hayo ili polisi waweze kufanya kazi zao kwa wakati?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sikudhani Yassini Chikambo, Mbunge wa Viti Maalum, kama lilivyoulizwa kwa niaba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Ruvuma una jumla ya magari 33 na kati ya hayo magari 24 ni mazima yanafanya kazi na magari tisa ndiyo mabovu. Aidha, Jeshi la Polisi hufanya mgao wa magari katika mikoa na vikosi kwa kuzingatia vigezo mbalimbali kama kiwango cha uhalifu katika eneo husika, hali ya jiografia, idadi ya watu na mahitaji ya kiutawala ambapo katika mwaka 2015 Mkoa wa Ruvuma ulipokea magari 11. Hivyo, mpango wa kupeleka magari katika Mkoa wa Ruvuma utategemea upatikanaji wa magari mapya na mahitaji kulingana na vigezo vilivyoainishwa.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitenga na kupeleka mgao wa fedha katika Jeshi la Polisi kila mwezi ambapo fedha hizi hugaiwa na kupelekwa mikoani kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya jeshi ikiwemo operation, matengenezo ya magari na mafuta kwenye vituo vya polisi. Aidha, utaratibu ulipo sasa kila Mkoa unapelekewa fedha kwa ajili ya matengenezo na mafuta kila mwezi kupitia kasima ya mikoa. Ni kweli kuwa magari mengi kwa sasa yamekuwa ni ya muda mrefu hivyo huhitaji matengenezo ya mara kwa mara ambapo Jeshi la Polisi linahitaji kufanya matengezo kwa magari yanayoharibika kwa kutumia fedha zinazopelekwa na kuwashirika wadau wa ulinzi na usalama katika maeneo husika.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-
Kumekuwa na ajali nyingi zinazotokana na vitendo vya baadhi ya Askari Polisi maarufu kama PT kuwakamata waendesha bodaboda wakiwa kwenye mwendo huku wakiwa wamebeba abiria. Hali hiyo hupelekea waendesha bodaboda na abiria kupata ajali mara kwa mara:-
Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kuwa ajali za kizembe zinazosababishwa na baadhi ya Askari Polisi zinakomeshwa?
WAZIRI WA MAMBO NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa tafiti mbalimbali zilizofanywa na Jeshi la Polisi, ajali za barabarani husababishwa na vyanzo vikuu vitatu ambavyo ni vyanzo vya kibinadamu ambavyo husababisha ajali kwa asilimia 76, vyanzo vya kiufundi ambavyo vinasababisha ajali kwa asilimia 16 na vyanzo vya kimazingira ambavyo vinasababisha ajali kwa asilimia 8. Ni katika vyanzo vya kibinadamu ndivyo tunakuta kuna uzembe ambao pia uko wa namna nyingi.
Mheshimiwa Spika, baadhi ya vijana wetu waendesha pikipiki bado wana uelewa mdogo kuhusu sharia za usalama barabarani na wengine pikipiki zao zina mapungufu mengi ambayo huwafanya kutokujiamini wanapoendesha. Kutokana na sababu hizi na nyinginezo, waendesha pikipiki hujihisi wana makosa wakati wote wawapo barabarani na hivyo huwa na hofu ya kukamatwa na Askari Polisi.
Mheshimiwa Spika, ni wajibu wa Askari Polisi kuhakikisha kuwa sheria zinafuatwa na si kuvunjwa. Waendesha pikipiki wanapaswa kutambua hilo na wao kutimiza wajibu wao wa kufuata sheria. Hali ya kutambua kuwa wana makosa ndiyo huwafanya kukimbia askari hata kama askari hana lengo la kuwakamata, hivyo husababisha ajali za kizembe bila sababu.
Mheshimiwa Spika, ili kuepukana na ajali za kizembe, Serikali kupitia Jeshi la Polisi itaendelea kutoa elimu kwa waendesha pikipiki ili kuwajengea uelewa wa sheria za usalama barabarani. Elimu hii itasaidia kuondokana na dhana potofu iliyojengeka miongoni mwa waendesha pikipiki na wapanda pikipiki kutokutii sheria ama kusababisha vyanzo vya ajali barabarani kwa kuwakimbia Askari Polisi kwa hofu ya kukamatwa, hata kama hawana makosa.
Mheshimiwa Spika, aidha, natumia fursa hii pia kulielekeza Jeshi la Polisi nchini kutumia muda wao vizuri katika kuwaelimisha waendesha pikipiki kufuata sheria za usalama barabarani kwa ajili ya usalama wao na watumiaji wengine wa barabara.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Wananchi wa Jimbo la Mbeya Vijijini wanaipongeza Serikali kwa kuanzisha Wilaya ya Kipolisi Mbalizi.
• Je, ni lini Ofisi ya Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi pamoja na nyumba za askari zitajengwa?
• Je, Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi ina magari mangapi na Serikali ina mpango gani wa kuboresha miundombinu ya vituo vya polisi katika Halmashauri ya Wilaya Mbeya?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo:-
i. Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi ni miongoni mwa Wilaya Mpya za Kipolisi zilizoanzishwa hivi karibuni. Jeshi la Polisi kwa kutambua ukosefu wa Ofisi ya Mkuu wa Polisi wa Wilaya pamoja na nyumba za makazi ya askari linashirikiana na wananchi na wadau mbalimbali kujenga jengo la Ofisi ya Mkuu wa Polisi wa Wilaya ambalo linajumuisha Kituo cha Polisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa jengo hili umefikia hatua ya umaliziaji na changamoto iliyobaki ni ujenzi wa nyumba za kuishi askari.
ii. Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kipolisi ya Mbalizi ina magari matatu ambapo gari moja ni chakavu linahitaji matengenezo ili liweze kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya vituo vya Polisi katika Halmashauri ya Mbeya pamoja na kwingineko nchini kwa awamu kwa kutegemea rasilimali zilizopo na upatikanaji wa fedha.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO aliuliza:-
Katika Wilayani Tunduru kulikuwa na Kambi ya Jeshi ambayo pamoja na mambo mengine ilishughulika na ulinzi katika Vijiji vya Wenje na Makande vilivyopo mpakani na Nchi ya Msumbiji:-
i. Je, Serikali halioni haja ya kurudisha Kambi hiyo ya Jeshi Wilayani Tunduru?
ii. Kambi iliyokuwepo ilikuwa na hekta za ardhi zisizopungua 18,000, je, Serikali ina mpango gani wa kuendeleza maeneo hayo ambayo sasa yamekuwa vichaka?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Wziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sikudhani Chikambo kama ifautavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Ulinzi wananchi wa Tanzania liliweka kituo cha ulinzi cha Kombania ya sita ya 691 kikosi cha Jeshi (06/691 KJ) katika eneo la Chitanda, Wilayani Tunduru. Kutokana na sababu ambazo zilikuwa za msingi kwa wakati huo kituo hicho kilifungwa na eneo hilo likarudishwa rasmi kwa uongozi wa Serikali ya Wilaya ya Tunduru mwaka 1998. Aidha, mwaka 2006 eneo hilo liliombwa upya na JWTZ kwa uongozi wa Mkoa wa Ruvuma kwa ajili ya kuendelea kulitumia katika kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi yetu katika eneo hilo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa pamoja na Makao Makuu ya Jeshi linaandaa mpango kwa kutumia wataalam wake kuwatuma kwenda Wilayani Tunduru kwa kushirikiana na uongozi wa Wilaya ya Tunduru kutathmini na kulipima upya eneo hilo na kulifanyia mchakato wa kulimiliki kwa misingi ya sheria za ardhi zilizopo.
MHE. JESCA D. KISHOA Aliuliza: -

Je Serikali inatumia mikakati gani kudhibiti mapato yatokanayo na gawio kutoka kwenye makampuni ambayo Serikali inamiliki hisa chini ya 50%?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina ambaye ndiye msimamizi wa uwekezaji wa Serikali katika Taasisi na Mashirika ya Umma pamoja na Kampuni ambazo Serikali ina hisa chache, inadhibiti mapato yatokanayo na gawio kwa kuhakikisha kuwa kila kampuni ina sera ya gawio, kurejea kwa mikataba ya mauzo ya hisa katika kuhakikisha maslahi ya Serikali yanalindwa pamoja na kufanya chambuzi za mara kwa mara kuhusu utendaji wa taasisi hizo. Aidha, Serikali inauwakilishi kwenye bodi za wakurugenzi wa kampuni ambapo pamoja na mambo mengine husimamia maslahi ya Serikali kwenye kampuni ikiwa ni pamoja na malipo ya gawio.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati hii imeiwezesha Serikali kuongeza makusanyo yake ya gawio kutoka kampuni ambazo ina hisa chache kutoka shilingi bilioni 34.92 mwaka 2015/2016 hadi kufikia shilingi bilioni 155.10 mwaka 2020/2021.
MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza:-

(a) Je, ni nini sababu ya kuweka tozo ya ada ya tathmini ya asilimia moja kwa mkopaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ambapo asilimia 50 inalipwa kabla ya kuanza kufanya tathmini na asilimia 50 inalipwa baada ya mkopo kuidhinishwa?

(b) Je, ni kigezo gani kilisababisha tozo kuwa asilimia 1 na si vinginevyo?

(c) Je, mkopo usipoidhinishwa hiyo asilimia 50 ya asilimia moja iliyolipwa inarudishwa ama la?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, ada ya tathmini ya mikopo inayotozwa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania ni kwa ajili ya kulipia gharama za uchambuzi wa maombi ya mkopo ambayo ni pamoja na shajara, uhakiki wa mradi pamoja na dhamana ya mkopo.

(b) Mheshimiwa Spika, kigezo kinachotumika kutoza ada ya uchambuzi wa maombi ya mikopo ni gharama halisi za uchambuzi wa maombi ya mkopo zinazotokana na nguvu ya soko kwa wakati husika. Aidha, utaratibu huu ni wa kawaida kwa taasisi za fedha kutoza ada ya uchambuzi wa maombi ya mikopo.

(c) Mheshimiwa Spika, endapo mkopo hautaidhinishwa, asilimia 50 ya asilimia moja iliyolipwa huwa hairejeshwi kwa mwombaji wa mkopo kwa kuwa kiasi hicho kinakuwa kimetumika kulipia gharama za uchambuzi wa mkopo.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kusamehe kodi za miaka ya nyuma taasisi za dini 7 zilizokuwa zikiendeshwa kwa utaratibu usiolenga kupata faida na kuziwekea utaratibu taasisi hizo kuanza kulipa tangu walipojulishwa kutakiwa kulipa kodi?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa sheria za kodi, taasisi za dini ambazo zinajiendesha kutokana na sadaka kutoka kwa waumini wao ama misaada inayotolewa na taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi, hazikatwi na hazitakiwi kulipa kodi ya mapato, isipokuwa taasisi zenye sifa kama hizo husajiliwa na kupewa Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) kwa madhumuni ya kuziwezesha kushughulikia masuala mbalimbali yanayohusu Mamlaka ya Mapato kama vile kuwasilisha kodi zinazokatwa kutoka kwa watumishi wa taasisi hizo na usajili wa mali mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, aidha, taasisi za dini zinazofanya shughuli za kiuchumi kwa lengo la kujipatia faida kutokana na shughuli hizo zinatakiwa kusajiliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania kama wafanyabiashara wengine na kulipa kodi ya mapato kulingana na faida inayopatikana.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikipokea maombi ya kusamehe kodi za miaka ya nyuma kutoka taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na taasisi za dini. Serikali inaendelea kutathmini maombi hayo ili kuona hatua zinazoweza kuchukuliwa bila kuathiri matakwa ya sheria zilizopo.
MHE. JERRY W. SILAA aliuliza:-

(a) Je, ni taasisi ngapi zilizo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango hadi sasa hazina Bodi au Bodi zake zimemaliza muda wake?

(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha benki ya waliopekuliwa ili muda wowote uteuzi ufanyike haraka kusaidia Taasisi hizo kwenda na kasi ya Mheshimiwa Rais kwani kwa sasa upekuzi imekuwa kisingizio cha kuchelewesha uteuzi?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry William Silaa, Mbunge wa Ukonga lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha na Mipango ina jumla ya Taasisi 28 ambazo inazisimamia na kati ya hizo Taasisi tisa Bodi zake zimemaliza muda wake na mapendekezo ya majina kwa ajili ya kujaza nafasi za Wenyeviti na Wajumbe wa Bodi hizo yamewasilishwa kwenye Mamlaka za Upekuzi.

Mheshimiwa Spika, upekuzi kwa ajili ya kujaza nafasi mbalimbali hufanyika kwa wakati husika kutokana na ukweli kwamba utendaji na mienendo ya maafisa hubadilika kutoka wakati mmoja hadi mwingine. Hivyo, siyo sahihi kuwa na kanzidata ya upekuzi (benki ya waliopekuliwa) ili kurahisisha mchakato wa upekuzi kwa kuwa utendaji na mienendo ya maafisa hubadilika kuendana na wakati husika.
MHE. JERRY W. SILAA aliuliza:-

(a) Je, ni taasisi ngapi zilizo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango hadi sasa hazina Bodi au Bodi zake zimemaliza muda wake?

(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha benki ya waliopekuliwa ili muda wowote uteuzi ufanyike haraka kusaidia Taasisi hizo kwenda na kasi ya Mheshimiwa Rais kwani kwa sasa upekuzi imekuwa kisingizio cha kuchelewesha uteuzi?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry William Silaa, Mbunge wa Ukonga lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha na Mipango ina jumla ya Taasisi 28 ambazo inazisimamia na kati ya hizo Taasisi tisa Bodi zake zimemaliza muda wake na mapendekezo ya majina kwa ajili ya kujaza nafasi za Wenyeviti na Wajumbe wa Bodi hizo yamewasilishwa kwenye Mamlaka za Upekuzi.

Mheshimiwa Spika, upekuzi kwa ajili ya kujaza nafasi mbalimbali hufanyika kwa wakati husika kutokana na ukweli kwamba utendaji na mienendo ya maafisa hubadilika kutoka wakati mmoja hadi mwingine. Hivyo, siyo sahihi kuwa na kanzidata ya upekuzi (benki ya waliopekuliwa) ili kurahisisha mchakato wa upekuzi kwa kuwa utendaji na mienendo ya maafisa hubadilika kuendana na wakati husika.
MHE. CECILIA D. PARESSO aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kudhibiti mfumuko mkubwa wa bei za bidhaa ulioanza tangu Desemba, 2020 ambao umefanya gharama za maisha kupanda?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mfumuko wa bei ulipanda kutoka asimilia 3.2 mwezi Desemba 2020 hadi asilimia 3.5 mwezi Januari 2021. Hii ilitokana na upungufu wa baadhi ya bidhaa sokoni ambao hutokea mara kadhaa katika vipindi vya mwanzo wa mwaka kama hivyo.

Aidha, mfumuko wa bei ulishuka na kufikia asilimia 3.3 mwezi Februari 2021 ikiashiria kuwa bidhaa na huduma zilianza kupatikana kwa bei nafuu kulinganisha na mwezi Januari mwaka uliopita.

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa mfumuko wa bei unaendelea kubaki ndani ya wigo wa tarakimu moja kati ya asilimia 3.0 hadi 5.0. Lengo hili linaweza kufikiwa kutokana na mikakati mbalimbali ya Serikali ikiwa ni pamoja na kuimarisha usambazaji wa chakula kutoka maeneo ya uzalishaji hadi katika maeneo ya walaji, kuimarisha usimamizi wa Sera ya Fedha na bajeti na kuboresha miundombinu ya barabara za vijijini ili kurahisisha usafirishaji wa mazao kutoka mashambani hadi katika masoko.
MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: aliuliza: -

Kumekuwa na kawaida kwa baadhi ya Taasisi za Serikali kutotumia huduma za Shirika la Bima la Zanzibar kwa kisingizio kuwa shirika hilo siyo la Umma.

(a) Je, Serikali inalitambua shirika hilo kama la Serikali au shirika binafsi?

(b) Kama ni shirika la Serikali, nini wito wa Serikali kwa watendaji ambao wamekuwa wakikataa kutumia huduma hiyo kwa kisingizio cha kuwa siyo shirika la Serikali?
NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, Mbunge Viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Bima la Zanzibar yaani Zanzibar Insurance Corporation limesajiliwa kwa mujibu wa Sheria ya Bima Namba 10 ya mwaka 2009 na lina leseni hai yenye usajili Na.00000704 inayoruhusu Shirika hilo kufanya biashara ya bima za kawaida yaani Non-Life Insurance. Shirika hilo linamilikiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa asilimia 100. Hivyo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua kuwa shirika hilo ni mali ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sio Shirika binafsi.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Shirika la Bima la Zanzibar ni mali ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, wito wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa watendaji ambao wamekuwa wakikataa kutumia huduma zake kuendelea kulitumia shirika hilo kwa ajili ya kupata huduma za bima kama ambavyo wanalitumia Shirika la Bima la Taifa hasa ukizingatia kuwa biashara ya bima nchini ni biashara Huru na Huria inayosimamiwa na Sheria ya Bima Namba 10 ya mwaka 2009 pamoja na Kanuni zake. Ahsante. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Tanzania ina idadi ya watu takribani milioni hamsini na tano wenye madaraja tofauti ya uchumi: -

Je, katika idadi hiyo Tanzania ina mabilionea wangapi?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia utafiti uliofanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania kwenye mwaka wa fedha 2014/2015 na baadaye kurejewa mwaka 2019/2020, unaonesha kuwa idadi ya mabilionea duniani inakadiriwa kufikia watu milioni kumi na nne. Kwa mujibu wa Ripoti ya Capgemini and RBC Wealth Management, July 2019. Bara la Afrika pekee lina mabilionea 140,000 sawa na asilimia moja ya mabilionea wote wa dunia nzima. Kati ya idadi ya mabilionea waliopo Barani Afrika, mabilionea 5,740 wanatoka Tanzania ambao wanamiliki asilimia 4.2 ya utajiri katika kundi la mabilionea wa Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha miongoni mwa mabilionea 5,740 waliopo Tanzania, mabilionea 115 sawa na asilimia mbili ya utajiri wa zaidi ya dola milioni 30 wanaomiliki zaidi ya asilimia 28 ya utajiri wote wa mabilionea wanaotoka Tanzania. Kati ya hawa mabilionea waliopo Tanzania wengi wamesajiliwa na Mamlaka ya Mapato yaani TRA na wanalipa kodi zao katika Idara ya Walipa kodi Wakubwa na wamewekeza katika Sekta za Viwanda, Nishati na Madini ikiwemo pia Sekta ya Fedha, Mawasiliano pamoja na Uchukuzi, Utalii na Makazi.
MHE. HASSAN S. MTENGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itashughulikia urejeshwaji wa Fedha za Wananchi wa Jimbo la Mtwara Mjini ambao walijiunga na Pride kwa ajili ya kupata mkopo?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Mtwara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama inavyokumbukwa kuwa kulikuwa na shauri mahakamani lililofunguliwa mwaka 2016 kuhusu umiliki wa Kampuni ya Pride; baada ya kukamilika kwa shauri hilo na kutolewa hukumu tarehe 11 Novemba, 2018 kuwa Kampuni ya Pride Tanzania ni mali ya Serikali, Serikali ilifanya tathmini ya hali ya kampuni na kufuatiwa kwa ukaguzi maalum uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kutambua kuwa mali na madeni ya Kampuni hiyo ambapo taarifa ilionesha kuwa Kampuni hiyo ina madeni makubwa kuliko mali zilizopo.

Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa hiyo, Wizara ya Fedha na Mipango imeielekeza Ofisi ya Msajili wa Hazina kusimamia ufilisi wa Kampuni hiyo kwa kufuata taratibu za ufilisi wa Makampuni. Hivyo, kwa sasa Kampuni ya Pride ipo katika hatua za ufilisi. Madai yote yanayohusu Kampuni hiyo yatashughulikiwa kwa kufuata taratibu za ufilisi.
MHE. LUHAGA J. MPINA aliuliza: -

Je, ni nini kinachosababisha kesi 1,097 za kodi za muda mrefu zenye thamani ya shilingi trilioni 360 na dola za Marekani milioni 181.4 kutoamuliwa hadi sasa?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, Mbunge wa Kisesa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali haina kesi 1,097 za kodi za muda mrefu zenye thamani ya shilingi trilioni 360 na dola za Marekani milioni 181.4 ambazo hazijaamuliwa. Aidha, hadi Agosti, 2022 kulikuwa na mashauri 854 kwenye hatua mbalimbali za usikilizaji yenye kodi inayobishaniwa ya jumla ya shilingi 4,207,442,214,759.93 (trilioni 4.21) na dola za Marekani 3,480,867.96 (milioni 3.48) katika Bodi ya Rufaa za Kodi na Baraza la Rufaa za Kodi.

Hivyo, kwa sasa taasisi za rufaa za kodi zinaendelea kusikiliza mashauri hayo pamoja na mashauri mapya yanayoendelea kusajiliwa. Vilevile kwa nyakati tofauti, idadi ya mashauri ya kodi hupungua au kuongezeka kulingana na kasi ya usikilizaji na usajili.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA K.n.y. MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza: -

Je, ni makundi gani yamenufaika na mkopo wa shilingi trilioni moja iliyoahidiwa kutolewa na Serikali katika sekta ya kilimo na kwa masharti gani?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania ilichukua hatua za ziada za kisera, ikiwemo kuanzisha dirisha la mkopo maalum la shilingi trilioni moja kwa benki na taasisi za fedha nchini ili kuchochea mikopo nafuu kwa sekta binafsi, hususan sekta ya kilimo. Masharti ya mkopo maalum ni kuchochea mnyororo wa thamani katika kilimo cha mazao, miundombinu ya umwagiliaji, mifugo, uvuvi na ununuzi na usindikaji wa mazao kwa wakulima wadogo na wa kati pamoja na kampuni ndogo ndogo na za kati. Aidha, benki na taasisi za fedha zinatakiwa kutoa mkopo usiozidi shilingi bilioni moja kwa kila mkulima kwa riba ya asilimia chini ya asilimia 10.

Mheshimiwa Spika, masharti mengine ni Benki Kuu kuzikopesha benki na taasisi za fedha kwa riba ya asilimia Tatu ili taasisi hizo kukopesha wakulima na kampuni zinazojishughulisha na mnyororo wa thamani katika sekta ya kilimo kwa riba isiyozidi asilimia 10. Aidha, hadi tarehe 31 Desemba, 2022, jumla ya mkopo wa shillingi billioni 164.9 umetolewa kwa sekta ya benki na taasisi za fedha na kuwanufaisha wakulima wadogo na wakulima wa kati zaidi ya 5,385 na AMCOS 21.
MHE. SALIM MUSSA OMAR aliuliza: -

Je, kuna Mwongozo unaosema kuwa Zanzibar Insurance Corporation haipaswi kushiriki kukata Bima za Miradi mikubwa?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI K.n.y. WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Omar Salim, Mbunge wa Gando, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Bima la Zanzibar (Zanzibar Insurance Corporation) limesajiliwa kwa kupewa leseni Na. 00000821 na Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) chini ya Sheria ya Bima Na. 10 ya Mwaka 2009. ZIC inafanya biashara za bima sehemu zote Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, biashara ya bima nchini ni huria na inaendeshwa kwa jumla ya makampuni 31 ya bima ikiwemo ZIC. Aidha, kampuni zote zina haki sawa ya kutoa kinga ya majanga kwa miradi mbalimbali Tanzania Bara na Zanzibar. Hivyo, hakuna Mwongozo wowote unaokataza Zanzibar Insurance Corporation kushiriki katika biashara ya kukata bima za miradi mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muktadha huo, Shirika la Bima la Zanzibar (ZIC), kama ilivyo kwa kampuni nyingine yoyote ya bima iliyosajiliwa chini ya Sheria ya Bima Na. 10 ya Mwaka 2009, inaruhusiwa kuweka kinga ya bima kwa miradi mikubwa. Ahsante.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza: -

Je, kuruhusu Benki kuwa Wakala wa Bima Serikali haioni kuwa Mawakala wengine watafunga biashara kwa kukosa wateja?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) pamoja na wadau wa bima ilianzisha BenkiWakala wa Bima ili kuongeza wigo wa usambazaji na upatikanaji wa huduma za bima kwa wananchi. Idadi ya Mawakala wa Bima wa Kawaida imekuwa ikiongezeka sambamba na BenkiWakala wa Bima kwa sababu hali hii imechochea ushindani, ubunifu na kutegemeana. Takwimu zinaonesha BenkiWakala waliosajiliwa kwa mwaka 2020 wako 14; mwaka 2021 wako 23; mwaka 2022 wako 27; na hadi 30 Machi, 2023 walishafika 30. Aidha, Mawakala wa Bima wa Kawaida waliosajiliwa kwa mwaka 2020 walikuwa 745; mwaka 2021 walikuwa 789; mwaka 2022 walikuwa 910; na kwa mwaka 2023 hadi Machi, 2023 wameshafika 960.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa takwimu hizi, ni dhahiri kuwa Mfumo wa BenkiWakala wa Bima umesaidia kukuza biashara ya Bima hapa nchini.
MHE. MOHAMED SAID ISSA aliauliza: -

Je, hesabu zinazowasilishwa na CAG kila mwaka ni za mashaka au uhakika?
WAZIRI WA FEDHA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohammed Said Issa, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hesabu zinazowasilishwa na Maafisa Masuuli kwa CAG kila mwaka ni za uhakika kwa kuwa zinaandaliwa kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 30(2) cha Sheria ya Fedha za Umma, Sura 348, Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu katika Sekta ya Umma (IPSAS), miongozo mbalimbali inayotolewa na Wizara ya Fedha na mifumo madhubuti ya kielektroniki ya usimamizi wa fedha ikijumuisha Mfumo wa Uhasibu Serikalini (MUSE).

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita (2019/2020 – 2021/2022), taarifa ya CAG imeonesha ongezeko la hati zinazoridhisha kutoka asilimia 92 mpaka 96 kwa Serikali Kuu, asilimia 70 mpaka 94 kwa Serikali za Mitaa na kupungua kutoka asilimia 97 mpaka 98 kwa Mashirika na Taasisi nyingine za Umma.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA aliuza: -

Je, kuna mpango gani wa kuongeza thamani ya shilingi ya Tanzania ikilinganishwa na nchi jirani za Afrika Mashariki?
WAZIRI WA FEDHA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kulinda thamani ya shilingi ya Tanzania kwa hatua zifuatazo: -

(i) Kushirikisha sekta binafsi katika kuimarisha mikakati ya kuongeza mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi;

(ii) Kuhimiza wananchi kuongeza matumizi ya bidhaa na huduma zinazozalishwa hapa nchini ili kupunguza mahitaji ya fedha za kigeni;

(iii) Kusimamia kwa karibu wazalishaji wa ndani ili kuongeza ubora katika uzalishaji wa bidhaa na huduma kwa lengo la kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi;

(iv) Kuendelea kusimamia utekelezaji wa kifungu 7(3) na 13(1) cha Kanuni za Fedha za Kigeni za mwaka 2022, zinazoelekeza wafanyabiashara kuweka katika benki zilizopo nchini fedha za mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi ndani ya siku 90 tangu siku ya kusafirisha bidhaa au kutoa huduma na wafanyabiashara wanaoagiza bidhaa kutoka nje kufanya malipo kwa kutumia benki na taasisi nyingine za fedha zilizopo nchini;

(v) Kuongeza vyanzo vya upatikanaji wa fedha za kigeni ikiwemo ununuzi wa dhahabu;

(vi) Kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji kutoka nje; na

(vii) Kusimamia utekelezaji wa sera ya fedha ili kuhakikisha utulivu wa mfumuko wa bei hapa nchini.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza:-

Je, kwa kodi ya mapato kwa wachimbaji wadogo wa madini isiunganishwe na Mineral Market Management Information System (MMMIS)?
WAZIRI WA FEDHA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze sana Taifa Stars jana kwa kutuandikia historia kubwa sana. Kiongozi akiwa na baraka malango yote yanafanyika, kila linalofanyika kwa sababu ya baraka za Mama Samia linakubali tu ndiyo maana hata Yanga tukaingia makundi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya awali, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathani Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kufuatia maelekezo ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuzitaka taasisi za umma kuhakikisha mifumo yote ya mapato na matumizi inasomana, Mamlaka ya Mapato Tanzania inaendelea kuunganisha na kufungamanisha mifumo yake ya usimamizi wa mapato na mifumo ya taasisi nyingine ikiwemo mifumo ya Mineral Market Management Information System.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Mamlaka ya Mapato Tanzania na Tume ya Madini zimeingia makubaliano ya kubadilishana taarifa ili kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato ya kodi na yasiyo ya kodi. Aidha, kodi ya mapato kwa wachimbaji wadogo wa madini inakusanywa katika masoko ya madini chini ya usimamizi wa Tume ya madini kwa niaba ya Mamlaka ya Mapato Tanzania.
MHE. NDAISABA G. RUHORO K.n.y. MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza:-

Je, nini mpango wa Serikali katika kunusuru uchumi wa nchi kutokana na ukosefu wa fedha za kigeni, hususani Dola ya Kimarekani?
WAZIRI WA FEDHA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za muda mfupi, wa kati na za muda mrefu katika kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa fedha za kigeni, hususani dola ya Kimarekani hapa nchini. Changamoto hiyo imesababishwa na athari za mgogoro wa vita kati ya Ukraine na Urusi; kuimarika kwa shughuli za kiuchumi na kijamii baada ya UVIKO-19; na mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ni utekelezaji wa sera za fedha ambayo inalenga kupunguza ukwasi katika uchumi wa nchi mbalimbali ikiwemo Marekani katika kukabiliana na masuala ya mfumuko wa bei. Kwa ujumla matukio hayo yameathiri mnyororo wa uzalishaji, usambazaji na uhitaji wa bidhaa na huduma katika soko la dunia.

Mheshimiwa Spika, hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kupunguza athari na changamoto za upatikanaji wa fedha za kigeni ni pamoja na:-

(a) Kuongeza kiwango cha kuuza fedha za kigeni katika soko la fedha za kigeni, ambapo kati ya Machi, 2022 na Agosti, 2023 Benki Kuu ya Tanzania imeuza katika soko la fedha za kigeni zaidi ya dola za Kimarekani milioni 500;

(b) Kuongeza vyanzo vya upatikanaji wa fedha za kigeni ikiwemo ununuzi wa dhahabu;

(c) Kutekeleza mikakati ya kuongeza mauzo ya nchi za nje na kuzalisha bidhaa mbadala wa zile zinazoagizwa kutoka nje ya nchi; na

(d) Kuendelea kushirikisha benki za biashara, maduka ya kubadilisha fedha za kigeni, pamoja na wadau wengine katika kuimarisha sheria, kanuni na miongozo mbalimbali ya usimamizi wa fedha za kigeni hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto zilizojitokeza, hali ya upatikanaji wa fedha za kigeni nchini imeendelea kuwa himilivu ambapo akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola za Marekani milioni 5,246.7 mwezi Julai 2023, kiasi kinachotosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa takriban miezi 4.7 ikilinganishwa na malengo ya miezi minne.
MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza:-

Je, nini utaratibu wa Serikali kutoa msamaha wa kodi ya jengo kwa wale wanaostahili baada ya kodi kuhamishiwa kwenye za LUKU?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutoa msamaha wa kodi ya majengo kwa wale wanaostahili unaendelea kutekelezwa kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa ya Utozaji wa Kodi ya Majengo Sura 289 ambapo mwenye jengo husika anatakiwa kuwasilisha maombi ya kupata msamaha wa kodi ya jengo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania. Baada ya TRA kujiridhisha kuwa muombaji anastahili msamaha kwa mujibu wa matakwa ya sheria, makato yake katika ununuzi wa umeme kupitia LUKU yatasitishwa. Aidha, kifungu cha 7(a) hadi (i) cha Sheria ya Serikali za Mitaa ya Utozaji wa Kodi ya Majengo, Sura 289, kimeainisha majengo yaliyosamehewa kulipa kodi ya majengo.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutoa msamaha wa kodi ya majengo umeainishwa katika Kanuni za Mamlaka za Serikali za Mitaa, Ukusanyaji wa Kodi ya Majengo, 2020 sehemu ya nne, Na. 16(1) hadi (6).

Mheshimiwa Spika, utozaji wa kodi ya majengo kupitia manunuzi ya umeme wa mfumo wa LUKU hauondoi haki ya msamaha wa kodi ya majengo kwa anayestahili kisheria bali umeongeza ufanisi katika kujiridhisha kuwa muombaji anastahili msamaha ili kuepuka kuwaondolea makato hata wanaostahili.
MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza: -

Je, nini utaratibu wa Serikali kutoa msamaha wa kodi ya jengo kwa wale wanaostahili baada ya kodi kuhamishiwa kwenye za LUKU?
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutoa msamaha wa kodi ya majengo kwa wale wanaostahili unaendelea kutekelezwa kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa ya Utozaji wa Kodi ya Majengo Sura 289 ambapo mwenye jengo husika anatakiwa kuwasilisha maombi ya kupata msamaha wa kodi ya jengo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania. Baada ya TRA kujiridhisha kuwa muombaji anastahili msamaha kwa mujibu wa matakwa ya sheria, makato yake katika ununuzi wa umeme kupitia LUKU yatasitishwa. Aidha, kifungu cha 7(a) hadi (i) cha Sheria ya Serikali za Mitaa ya Utozaji wa Kodi ya Majengo, Sura 289, kimeainisha majengo yaliyosamehewa kulipa kodi ya majengo.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutoa msamaha wa kodi ya majengo umeainishwa katika Kanuni za Mamlaka za Serikali za Mitaa, Ukusanyaji wa Kodi ya Majengo, 2020 sehemu ya nne, Na. 16(1) hadi (6).

Mheshimiwa Spika, utozaji wa kodi ya majengo kupitia manunuzi ya umeme wa mfumo wa LUKU hauondoi haki ya msamaha wa kodi ya majengo kwa anayestahili kisheria bali umeongeza ufanisi katika kujiridhisha kuwa muombaji anastahili msamaha ili kuepuka kuwaondolea makato hata wanaostahili.