Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Allan Joseph Kiula (38 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuweza kunipatia nafasi nami nichangie hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nachukue nafasi hii kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba yake. Hotuba hii imekaa vizuri kwa sababu imegusa maeneo yote ya utendaji kazi na maeneo yote ambayo ni matarajio ya nchi. Pia nampongeza Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa utendaji kazi wake mzuri. Wanasema unakunywa chai ya moto na andazi moto. Maana yake nini? Maana yake unatoa ahadi, unaanza kutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, elimu bila malipo imeanza kutekelezwa, changamoto zipo, inabidi sisi sasa tuziboreshe. Hotuba hii imejengwa katika msingi mzima wa Mipango ya Miaka Mitano. Kwa maana hiyo, imezingatia na ni hotuba ambayo ina tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo habari ya mapato. Ili kuweza kufanikisha utekelezaji wa mipango mbalimbali ambayo tunapanga ndani ya Bunge hili, ni lazima suala la mapato liangaliwe kwa kina. Ninapozungumzia mapato, maana yake ni nini? Maana yake ni lazima tupanue wigo wa mapato, tutafute vyanzo vipya vya mapato, tuachane na ule utamaduni wa kupandisha gharama kodi kwenye sigara, pombe lakini pia na kodi ya wafanyakazi. Lazima tupanue wigo wa mapato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kuna sekta isiyo rasmi. Sekta isiyo rasmi ni kubwa lazima tuirasimishe. Tukiirasimisha, wigo utapanuliwa, lakini pia wawekezaji wanaokuja kuwekeza ndani ya nchi yetu, inatakiwa tuziangalie kodi wanazostahiki kulipa. Kodi hizo zikiwekwa vizuri, tutapata mapato. Pia liko jambo ambalo na lenyewe sisi kama Wabunge inabidi tuliangalie. Yako mambo kwa sababu Sheria za Ukusanyaji wa Mapato zinatungwa na Bunge hili lakini imeshafikia mahali sisi Wabunge ndiyo tunazihoji. Sasa tunapozihoji, inakuwa ni changamoto kubwa.
Kwa hiyo, naomba Waziri anayehusika aje atuelimishe upya, hizi sheria zinazopitishwa hapa na zinazotumika. Kwa mfano, Sheria ya Uondoaji wa Mizigo Bandarini kwenda nje ya nchi, hizi transit goods; uamuzi ulifikiwa wa taratibu za kuondoa na ulipaji kodi, lakini wako watu ambao wanahoji na zilipita humu humu ndani. Sasa ni muhimu jambo hilo na sisi tukalielewa kwa sababu sisi kama Wabunge tunatakiwa tuwe Walimu na ndio tuwaelekeze watu wetu. Kwa sababu mtu wa kijijini hawezi kujua hayo mambo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa eneo hilo limeanza kuendeshwa na Clearing and Forwading, hao Mawakala wa Forodha. Haiwezekani! Kama sisi ni Wawakilishi wa wananchi lazima tulisimamie, kama sisi ni Wabunge, lazima tulisimamie na tuisaidie Serikali katika kutoa mwongozo na kuwaambia watu jambo lipi linatakiwa kufanyika. (Makofi)
Cha pili, nizungumzie ajira. Nitajikita zaidi kwenye maeneo ya vijijini. Zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wetu ni wakulima. Sasa tunapozungumza ajira na kilimo, ina maana kilimo kinatoa ajira kubwa kwa watu wetu wa vijijini na kwa wananchi wetu wa vijijini. Jambo la muhimu ni nini? Wananchi wetu wanatakiwa wapate mbegu bora kwa bei rahisi, wapate pembejeo kwa bei rahisi. Mambo hayo yakifanyika, tunaweza kuchangia kupanua wigo wa ajira badala ya kutegemea hizi wanaita white colour job au Ajira za kuajiriwa maofisini. Kilimo ni sekta kubwa ambayo inaweza ikatoa ajira. Ukiangalia ukurasa wa 28 suala hilo limezungumziwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 32 kuna suala la viwanda na kilimo. Ukienda kwa mfano Wilaya ya Mkalama, tunalima sana alizeti, vitunguu, mahindi na mazao mengine. Sasa lazima kuwe na muunganiko kati ya hii malighafi ambayo itakwenda viwandani. Kwa hiyo, kitu cha msingi zaidi ni kusisitiza suala la kilimo ambacho kitatoa malighafi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kilimo, kuna suala la masoko. Wananchi wetu lazima tuwatafutie masoko. Tunawatafutia masoko vipi? Kwa kutengeneza masoko ya kukukusanyia mazao, kwa sababu mwananchi ananyonywa sasa hivi. Kwa mfano, kule Mkalama, kuna mtu anatembea na debe linaitwa Msumbiji; debe nane kwa debe sita. Sasa mkulima anapunjwa. Kwa hiyo, tukiwa na sehemu za kukusanyia mazao, kwa Mfano Kibaigwa kuna soko la Kimataifa na sehemu kama Iguguno kunaweza kukawa na soko la Kimataifa la kuuza mazao tukawasaidi wakulima wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la ardhi. Maeneo mengi yamekuwa na migogoro ya ardhi ikiwemo Mkalama. Ipo migogoro mingi ya ardhi. Pia hao watu wanaokuja kupewa ardhi kubwa kubwa; kuna mtu anapewa ekari 700 na anapewa ndani ya kijiji, maana zinapimwa mpaka zinaingia ndani ya kijiji. Sasa hao wataalam wetu wanaona jambo hilo? Hilo ni jambo ambalo inabidi likemewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wilaya zinaanzishwa, hakuna Afisa Ardhi Mteule. Nalo ni changamoto kubwa. Kwa hiyo, naomba Ofisi hii iangalie, kuwe na Maafisa Ardhi Wateule. Wilaya inapoanzishwa, ateluliwe Afisa Ardhi Mteule na Hakimu wa Wilaya ili mambo yaweze kusonga mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la barabara. Hapa ndiyo ipo changamoto kubwa. Maana tunapozungumza suala la barabara, mimi huwa naangalia, wenzetu wa Dar es Salaam barabara zote ni lami, lakini ukienda Mkalama na maeneo mengine ya pembezoni barabara zote ni vumbi; na uwezo wa Halmashauri zetu wa kukusanya mapato ni mdogo sana. Kupandisha hadhi barabara ya Halmashauri yenyewe ni changamoto, acha kupandisha iwe barabara ya TANROAD.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala hilo linatakiwa liangaliwe kwa makini. Zipo barabara kwa mfano kutoka Mwangeza mpaka Endasiku, zipo barabara za kwenda Iramoto, zile hazipo kabisa kule ni mapalio tu, lakini maeneo hayo ndiyo yanayozalisha mazao kwa wingi kama alizeti na mahindi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nachukua nafasi hii kwa kuipongeza Serikali kwa kutoa pesa daraja la Sibiti kuanza kujengwa. Hapo ndipo sera ya kuunganisha Mkoa kwa Mkoa wa Singida na Simiyu, tutapata unafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona wamesema maji vijijini yamesambazwa kwa asilimia 72, lakini nikiangalia vijiji vyangu vyote havina maji, halafu asilimia 72 imetokea vipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Waziri mhusika anatakiwa angalie jambo hili, iko miradi ambayo imefadhiliwa na Benki ya Dunia, haijamaliza; lakini inahesabika kwamba mradi upo na unafanya kazi. Wahandisi ni wa aina gani? Bomba za maji zinapita mtoni. Mto unakuja unazoa maji pale Iguguno, unasema mradi wa World Bank. Mradi wa World Bank lazima uwe na hadhi ya World Bank, siyo unakuwa mradi kama wa kimachinga tena. Kwa hiyo, Waziri wa Maji anatakiwa aangalie matumizi ya pesa na watu wapate maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya mpya zina changamoto kubwa; Hospitali za Wilaya hazipo! Kama hazipo, Halmashauri ikijitahidi hata ikiweka kwenye mpango haiwezi, kwa sababu kipato ni kidogo. Wilaya hizi ziangaliwe kwa jicho la karibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ulinzi na usalama. Jeshi la Polisi na wengine lazima waangaliwe kwa karibu. Sisi tunaokaa porini kule, amezungumza Mheshimiwa Musukuma huko, watu wanakatwa mapanga tu! Kwetu, vijana wa bodaboda wanatekwa tu! Suala la ulinzi lazima liangaliwe, magari na mafuta yapelekwe ili tuweze kupiga hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Wilaya mpya na wenyewe ni changamoto. Kwa mfano, Wilaya ya Mkalama, mwaka 2014 ilitengewa shilingi bilioni moja ikapewa Shilingi milioni 450; mwaka huu ilitengewa shilingi bilioni moja, haijapelekwa hata senti tano! Hiyo Wilaya mpya itakwisha lini? Hiyo na yenyewe ni changamoto kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, niipongeze tena hotuba ya Waziri Mkuu, naunga hoja mkono, tushikamane. Watu walikuwa wanataka maamuzi magumu, haya ndiyo maamuzi magumu. Ukiangalia maeneo yote yaliyotumbuliwa, yameguswa maeneo ambayo hayajawahi kuguswa. Sasa maeneo hayo yaliyoguswa, wameguswa ndugu zetu, kaka zetu; tuvumilie! Tunataka kujenga Tanzania mpya. Utajengaje Tanzania mpya kama huchukui hatua? Nashukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kukupa shukrani kwa kunipatia nafasi ya kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu jioni ya leo. Nachukua nafasi hii kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na timu yake kwa reforms ambazo zinaendelea katika Sekta ya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza Mbunge aliyepita hapa kwamba ukienda Muhimbili unaona mabadiliko na ziko sehemu nyingi ambapo ukienda unaona mabadiliko; nami nafananisha utendaji kazi wa Rais wetu na Mawaziri hawa kama ile theory ya Japan, “Gemba Kaizen Theory,” ambayo inasema lazima uende kwenye gemba. Lazima uende mahali shughuli zinapofanyika ili uweze kutoa majibu sahihi kwa changamoto sahihi ambazo zinakuwepo…
Ni sababu ya urefu jamani, samahani! Nitakuwa napiga magoti. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema kwamba, utendaji kazi wa Waziri na Mawaziri umechukua ile theory ya Japan, inaitwa Gemba Kaizen Theory ambayo inasema uende kwenye eneo la tukio ili uweze kutatua matatizo. Unaona changamoto, unatatua matatizo hayo. Pia nawapongeza Madaktari na Wauguzi ambao wameendelea kufanya kazi bila kuchoka kwa weledi mkubwa kuokoa maisha ya Watanzania tukitambua kwamba population yetu sasa hivi ni zaidi ya milioni 48, hivyo tunahitaji kupata huduma hiyo muhimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizungumzie suala la haki ya kupata tiba. Suala la haki ya kupata tiba ni sawa sawa na haki ya kuishi, kwa sababu ukipata tiba ina maana unaendelea na maisha. Sasa nikiwahamisha Bunge hili nilipeleke katika Jimbo langu la Mkalama, tunao wakazi 188,000. Wakazi hao hawana Hospitali ya Wilaya, tunatumia Hospitali ya Mission. Vituo vya Afya vilivyopo ni vitatu, Zahanati zilizopo ni 24. Facilities hizo ndizo zinatoa huduma kwa idadi hiyo ya wakaazi. Wakaazi hao wako kwenye remote area, yaani maeneo ya pembezoni. Tunaposema maeneo ya pembezoni, maana yake unaondoka kwenye njia kuu za lami unaingia porini, ukiingia porini ndiyo unawakuta hawa wananchi wa Mkalama ambapo wako ndani katika vijiji vinavyofikia 70.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza vifo vya akinamama, watoto na wazee takwimu tunazozisoma humu kwenye vitabu hivi tunavyoandikiwa zinajumuisha vile vifo vinavyorekodiwa kutoka kwenye Hospitali, Zahanati na Vituo vya Afya. Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba vipo vifo vingi ambavyo havitolewi taarifa kwa sababu watu wanafariki majumbani. Akinamama wanafariki njiani wakienda kujifungua. Ukiangalia sisi huduma tunategemea Hospitali ya Hydom kupata matibabu. Ukitoka hapo unaenda Nkhungi, lakini unaenda Singida; na Jimbo lilivyo kubwa huduma hiyo haipatikani kwa urahisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba kabisa Wizara iangalie Wilaya hizi mpya na iangalie maeneo ya pembezoni yapate uangalizi wa karibu. Pia kwa kutambua wingi wa watu na Kata; tuna Kata 17; naomba kupitia Wizara hii Zahanati zifuatazo zipandishwe ziwe Vituo vya Afya. Ihuguno, Msiu, Nduguti na Ilunda. Tukipandisha hivyo, tutakuwa na Vituo vya Afya saba. Pia tunalo gari la wagonjwa moja ambapo gari hilo ni chakavu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wasiotambua ni kwamba sisi tumegawanyika kutoka Iramba Magharibi, ndiyo tukapata Iramba Mashariki. Kwa hiyo, tuligawiwa gari moja. Hatuna gari la wagonjwa. Tunalo gari chakavu ambalo halina uwezo tena wa kufanya kazi. Kwa hiyo, namwomba kabisa Waziri anayehusika na Wizara hii na Naibu wake waangalie uwezekano wa kutupatia gari la wagonjwa na gari hilo liwe jipya kwa sababu ya mazingira ya kwetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia suala la watumishi; tunao Madaktari wawili, watu 188,000 ukigawanya kwa Daktari wawili unapata 94,000; ukigawanya unakuta kwamba kila Daktari anahudumia watu 257 kwa siku katika siku za mwaka ukigawanya. Madaktari hawa watafanyaje kazi kwa utaratibu huo? Nasi kule tunaposema Madaktari, maana yake hata ma- clinical officer ni Madaktari. Maana yake hapo wenzetu wanapozungumza Madaktari wanazungumzia Madaktari Bingwa, lakini tunaoishi nao kule ni akina nani? Tuna upungufu wa Madaktari 21, Wauguzi 113 na Maabara 23. Tunaomba ufanyike mpango mahsusi tuweze japo kupunguziwa pengo hilo la wafanyakazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali yetu ya Nkhungi ambayo ni ya Mission na yenyewe iweze kupelekewa Madaktari Bingwa waweze kuendelea kutoa huduma wakati ambapo tunasubiri mabadiliko zaidi ambayo tunatarajia tutayapata ndani ya miaka mitano hii. Pia ukiangalia sasa hivi kuna magonjwa yasiyoambukiza (non communicable disease), sasa kule vijijini watu wanapokuja huku mijini kupata huduma wanakuwa wameshachelewa. Cancer, fibroid, sukari, BP, Cardiovascular Disease, magonjwa ya figo, hayo yote ni matatizo makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kabisa, uwe unafanyika utaratibu maalum kuwa na mobile health services au Kit Program za Madaktari; wanapelekwa, wanatembelea wilaya hizo na kuwapima watu na kuwasaidia, hasa akinamama ambao ndiyo waathirika wakubwa. Program hizo zikiwa zinafanyika katika kipindi cha miezi mitatu mitatu, zinaweza kutusaidia sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala ambalo limezungumzwa na kila Mbunge hapa linaloitwa CHF. CHF ni tatizo kubwa! Tunasema ni tatizo kubwa kwa sababu tunawahamasisha wananchi wanachanga, wakimaliza kuchanga hawapati matibabu na mwaka ukiisha wanatakiwa wachange tena. Sasa hivi tunatakiwa tuwaambie wananchi wachange na dawa hawakunywa; hiyo ni changamoto kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara iweze kuangalia jambo hili na kuweka utaratibu mzuri kuhakikisha wananchi wakitoa hizo fedha wapate dawa. Dawa ziwepo wapate na vipimo vinavyohusika, tumeambiwa kwamba dawa zikiwa hazipatikani MSD, kutakuwa na mzabuni kila mkoa. Jambo hilo Mkoa wa Singida halijafanyika na lenyewe liangaliwe ili dawa ziweze kupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maslahi ya wafanyakazi wa Wizara hii yaangaliwe kwa karibu kwa kuzingatia mazingira magumu. Sisi ambao tuko pembezoni, Madaktari wetu wanafanya kazi masaa 24 kwa siku saba, wanapata kitu gani cha ziada? Siyo hivyo tu, mgawanyo wa Madaktari hao; Madaktari wanaishia mijini. Wakifika Singida, wanageuka, wanarudi walikotoka au wanakwenda kwenye hospitali binafsi. Jambo hilo linatakiwa liangaliwe na Madaktari wafike kule kwa kuweka incentives mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la matibabu bure kwa wazee na lenyewe liangaliwe. Mheshimiwa Waziri ametoa circular, ipo, lakini haijasimamiwa kikamilifu. Bado malalamiko yako kila upande, wazee wetu wanapata tabu, wananyanyaswa. Wilaya ya Mkalama ni wilaya changa, mapato yake ni kidogo sana. Tunapofikia mahali tunasema wilaya ijenge hospitali, hiyo ni changamoto. Tunaomba Wizara itutafutie mfadhili au ichukue hatua za makusudi kuhakikisha kwamba tunapata Hospitali ya Wilaya ili iweze kutoa huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, alizungumza Mbunge mmoja suala la mafunzo, naomba Sekta ya Afya, Wizara iangalie namna kwenye Vyuo, wanafunzi hao waweze kupata mikopo, waweze kusoma, kwa ngazi ya cheti, ngazi ya Diploma na kwenda mpaka juu. Kwa sababu wakisoma na tukiweka mkakati wa miaka mitano, mpaka itakapokwisha, pengo hili litakuwa limemalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri na naomba mambo ambayo tumeyatoa yazingatiwe na hasa sisi ambao tunatoka katika maeneo ya porini. Mimi naita kule ni porini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi kuweza kuchangia hotuba hii. Pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Iramba Mashariki kwa kuweza kuniamini niweze kuwawakilisha badala ya wao 188,000 kuingia humu ndani ya Bunge.
Mheshimiwa Spika, ninapongeza hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, kwa maana mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, mambo mengi ambayo tuliyoyazunguza tuliyoyajadili kwenye Kamati yamepewa nafasi yake, ushauri umezingatiwa, kwa sababu ushauri umezingatiwa tunaamini kabisa kwamba utekelezaji wake utakuwa kama ulivyowasilishwa.
Mheshimiwa Spika, pia ninalipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kazi kubwa linayofanya na limetoa taswira nzuri ndani ya nchi na nje ya nchi. Tunapozungumza mambo ya ulinzi na usalama ni masauala nyeti. Tunasema masuala nyeti kwa sababu yuko Mbunge hapa alizungumza akasema maendeleo yoyote tunayoyategemea, maendeleo ya viwanda, maendeleo ya kilimo, huduma nzuri za afya, lazima usalama uwepo.
Mheshimiwa Spika, tumeona matukio ya kigaidi, matukio ya uharamia, vituo vya polisi kutekwa, lakini Jeshi la Wananchi wa Tanzania ni nguvu ya ziada ya kuweza kuhakikisha kwamba kunakuwepo na usalama ndani ya nchi yetu na Taifa linakuwa salama na tunaweza kufanya shughuli zetu kikamilifu.
Mheshimiwa Spika, mama akipika maandazi nyumbani watoto wakila na wakishiba unaweza ukakuta wanacheza mpira, sasa mambo yote haya tunayasema kwa sababu kuna amani na utulivu, tunatembea tunavyotaka, tunafanya mambo yetu tunavyotaka, ndiyo maana tunaweza tuka-undermine au tusione mchango wa Jeshi letu na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.
Mheshimiwa Spika, katika kuchangia nianze suala la ufinyu wa bajeti; ndani ya hotuba ya Waziri amezungumzia maombi ya fedha na ufinyu wa bajeti. Hilo ni jambo muhimu ambalo Serikali inatakiwa isikie na ione. Kwa sababu Jeshi linapopewa fedha ambazo hazitoshelezi ina maana haliwezi kutekeleza programu zake mbalimbali ambapo programu zote zinazowekwa kwenye bajeti huwa ni Strategic Program, programu ambazo zinaaminika kabisa zina mchango kwa Taifa hili kwa ujumla wake. Kwa hiyo, suala la bajeti ya Wizara linatakiwa liangaliwe kwa macho mawili au kwa ukaribu zaidi.
Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni suala la madeni. Tumeona kuna madeni karibu shilingi bilioni 483. Madeni hayo ni changamoto kubwa kwa Wizara, kama una madeni mengi namna hiyo au madeni makubwa kwa kiasi hicho hata moyo wa kutaka kutekeleza programu zingine unarudi nyuma kwa sababu ukipa fedha inabidi ulipe hayo madeni kwanza. Pia tunaposema madeni, Jeshi likidaiwa maana yake tunaathiri taswira ya Jeshi, kwa sababu Jeshi ni chombo ambacho hakitakiwi kudaiwa, ni chombo ambacho kinatakiwa kiwe salama salimini ili kiweze kuaminika na kiwe na taswira inayoeleweka. Kwa hiyo, nashauri kabisa, Wizara ya fedha iangalie namna ya kulipa madeni hayo ambayo mengine tunaambiwa ya kimkataba na hata madeni ya kimkataba yanapochelewa kulipwa ina maana yanatengeza riba, ina maana madeni hayo yatakua na kukua kwa maana hiyo, Jeshi litapata changamoto kubwa.
Mheshimiwa Spika, lakini jambo la tatu ambalo Wabunge wengine wameshalizungumzia ni maeneo ya Jeshi, ni muhimu maeneo ya Jeshi yote yakapimwa. Kwa hiyo, uchukuliwe mkakati wa maksudi wa kuhakikisha maeneo ya Jeshi yanapimwa, mipaka inafahamika siyo kwa wanajeshi tu na kwa wananchi wote na vijiji vinavyozunguka maeneo hayo, hiyo itasaidia kuondoa migororo ambayo tumekuwa tunaona inashamiri na inazidi kukua kwa sababu mgogoro unapokuwa mdogo, unapoona moshi ujue moto upo ndani yake. Kwa hiyo, lazima tuangalie namna ya kuondosha migogoro hii. Wakati tunasuburi fedha za kupima haya maeneo ni muhimu sasa Jeshi au Wizara ikachukuwa hatua ya kushirikisha vijiji husika kukawa na mazungumzo ya awali kuweka mipaka ya awali, kwamba baadaye tutapima mipaka hiyo, hapo tutakuwa tumeanza kutatua migogoro hiyo.
Mheshimiwa Spika, limezungumzwa suala la mafao ya askari wastaafu wa Jeshi. Wabunge wote tunasema yaanagaliwe upya, yapitiwe na wanajeshi wetu wasijione wanyonge, wametumikia, utumishi wao umekwisha, lakini sasa wanatakiwa waenziwe kwa utumishi wao na kwa amani ambayo wamekuwa wakiisaidia nchi hii kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Spika, iko changamoto ya maakazi ya askari, tumeona wanajenga nyumba 10,000 zimejengwa 4,000 bado haijapigwa hatua ya kutosha, ni muhimu ikatafutwa mikakati mingine ya ziada kuhakikisha kwamba askari wanakuwa na makazi yanayostahili.
Mheshimiwa Spika, kuhusu bajeti ya maendeleo. Mwaka huu tunasema kwamba asilimia 40 itakwenda kwenye bajeti ya maendeleo, lakini wenzetu wa Wizara hii wanayo miradi ambayo inahitaji kusukumwa kidogo sana ili iweze kusonga mbele. Kwa mfano, kuna mradi wa Mzinga, kile Kiwanda cha Mzinga kinaweza kufanya kazi kubwa, kikatoa bidhaa kwa ajili ya Jeshi la Polisi, Magereza na kikatoa hata kuuza nchi za jirani bidhaa zinazozalishwa pale, wenyewe wanaita mazao. Sasa ni muhimu kabisa mwaka huu wa fedha, fedha zikatolewa, idara hiyo ikaweza kujitegemea na ikasaidia katika maeneo mengine. Jambo hilo likifanyika litakuwa na mchango mkubwa.
Mheshimiwa Spika, tukizungumzia suala la afya, Jeshi lina hospitali zake, lakini kwenye hotuba ya Waziri tumeona wamezungumza kwamba pesa zinazotolewa hazikidhi na Waziri amefikia hatua ya kusema kwamba afya za wanajeshi zinakuwa mashakani, Sasa unapokuwa na wanajeshi wenye afya zilizo mashakani usalama huo utapatikana vipi?
Kwa hiyo, tunashauri kabisa kwamba pesa zilizotengwa mwaka huu ziende huko na zifanye kazi hiyo, wenzetu wamekuja na mbadala, mbadala wenyewe ni kwamba wanasema kuwe na aina ya bima ya afya, jambo hilo linatakiwa lifanyiwe kazi kwa haraka ili afya za askari ziweze kukaa vizuri.
Mheshimiwa Spika, kuna vyanzo vingine vya mapato ambavyo wenzetu wamezungumza, Mheshimiwa Azzan Zungu amezungumzia na msemaji mwingine amezungumza kuhusu UN Mission. Jambo kubwa tuliloliona ni kwamba UN Mission hizi hata zikienda vifaa havitoshi, kwa hiyo lazima tuweke mtaji wa kutosha, vifaa vinunuliwe ili tuweze kunufaika na hizo UN Mission. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, upo mradi wa mawasiliano ambao mwaka jana ulitekelezeka kwa kiwango kidogo sana, mwaka huu tunashawishi kabisa pesa zote zitolewe ili mradi huo wa mawasiliano uweze kukamilika.
Mheshimiwa Spika, kuhusu JKT, Wabunge tunashauri kwamba vijana kwanza wote waende JKT wanaostahili kwenda. Tunaposema wote waende maana yake nini, maana yake bajeti iongezwe waweze kwenda. Tuna SUMA JKT itumiwe kulinda Taasisi zote za Serikali na SUMA JKT walipwe, kwa sababu tumeona kwamba yapo madeni, wanalinda hawalipwi, maana yake nini? Nashauri kabisa kwamba wale wanaodaiwa, Wizara ichukue hatua za kupeleka madai yao kwa Mlipaji Mkuu ili pesa ziweze kukatwa juu kwa juu. Kwa sababu inaonekana zikishaingia kule basi kunakuwa na kiini macho ambacho kinaendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na mchango wangu ndiyo huo. Naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia japo kidogo katika hotuba ya Waziri. Nianze kwa kupongeza bajeti imetengenezwa vizuri, mahesabu tumeyaona lakini tunayo kazi ya kujaribu kutoa michango yetu panapotakiwa kurekebishwa parekebishwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, wamesema wenzangu jambo la faraja ni kwamba pesa hizi zote tunazokusanya asilimia 40 zinaenda kwenye miradi ya maendeleo, hilo ni jambo la faraja. Kingine cha msingi zaidi, niliwahi kufanya kazi TRA, jambo kubwa ambalo sisi tunapungukiwa ni utayari au utamaduni wa kulipa kodi, lakini ukitaka kitu chochote kizuri lazima ukigharamie. Kwa hiyo, inatakiwa tufikie mahali Watanzania tuone umuhimu wa kulipa kodi ili tuweze kupata maji, barabara na huduma nyingine ambazo tunahitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo ambalo napenda Wabunge pia walielewe na Waziri natumaini analifahamu, katika mwelekeo wa sasa hivi kodi za ndani zinatakiwa zichukue nafasi kubwa. Tumezoea hizi international taxes contribution yake percentage inakuwa kubwa, lakini ili tuweze kuendelea lazima kodi za ndani zikusanywe kikamilifu, tuone maeneo ambayo kodi zinaweza kupatikana kwa uhakika.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni watu walikuwa wanasema meli hazionekani bandarini, kodi imeshuka, maana yake nini? Ingekuwa kodi za ndani zimeimarika jambo hilo tusingekuwa tunalizungumza. Kwa hiyo, ni jambo muhimu ambalo inabidi tulione na tuisaidie Wizara na tuisaidie Serikali kuweza kubaini maeneo ya kupanua wigo wa kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuachane na mambo ya TRA na kadhalika nizungumzie kodi za majengo. Nimeshuhudia kulikuwa na mvutano wa jambo hili lakini nasema kama sisi ni Watanzania kabisa tusirudi nyuma, kodi za majengo zikusanywe na TRA. TRA wanazo resources za kutosha kwa maana wanao wafanyakazi wa kutosha, wanazo database, wanayo mifumo ambayo inaweza ika-support ukusanyaji wa kodi lakini pia itakusanywa kodi stahiki kwa maana kwamba kile ambacho kinatakiwa kukusanywa kitakusanywa. Wakati mwingine sisi huwa hatuambiani ukweli kwa sababu Halmashauri zetu zilishindwa hata kufanya valuation ya majengo ili kupanua wigo wa kodi. Sasa lazima tukitaka kodi ya majengo ipatikane tukubaliane valuation ifanyike, identification ya property ifanyike properly na tutapata pesa nyingi sana mpaka wenyewe mtashangaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukija kwenye vyanzo vingine vya mapato wamezungumza wenzangu suala la utalii. Nafikiri Mheshimiwa Waziri amelisikia, VAT kwenye utalii hiki kitakuwa ni kizungumkuti kwa sababu tunataka watalii waje, tunataka tuweke incentives mbalimbali na tunataka tuchukue opportunity ya usalama wa nchi yetu hii ili watalii waongezeke. Kwa hiyo, jambo hili inabidi liangaliwe kwa ukaribu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Tanzania ina wakulima wengi wanalima alizeti na pamba, suala la kutoza ushuru wa forodha wa asilimia kumi badala ya zero kwenye mafuta ghafi ya kula na lenyewe tuliunge mkono, libakie kama lilivyo ili tuweze kuwasaidia wakulima wetu waweze kupata masoko, viwanda vyetu vya ndani viweze na vyenyewe kusonga mbele. Kwa sababu ukiangalia sasa hivi mafuta ya alizeti hayana cholesterol, lakini hayauziki kwa sababu bei yake ni kubwa. Kwa kufanya hivyo, nafikiri tutapiga hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo jambo naomba tutafakari pamoja hapa na Mheshimiwa Waziri. Jambo lenyewe la kutafakari ni kwamba karibu kila Mtanzania ana simu, ukichukua population ya Watanzania, Mheshimiwa Zungu amezungumza hapa, lakini kodi za kwenye simu hazionekani. Ukienda hapa jirani Kenya (Safari Com) kila siku ya mlipa kodi Safari Com wapo, mchango wao ni mkubwa, kiwango kinachotolewa kinaonekana, Tanzania kuna tatizo gani? Hizi kampuni za simu zinakwepa vipi kulipa au zinaficha vipi mahesabu yao? Mimi naamini TRA wako wataalam lakini naamini utaalam huo unatolewa sisi hatuuchukui, ingekuwa tunachukua utaalamu huo tungekuwa tumeshapiga hatua kubwa mpaka ikiwepo kuishauri TCRA ku-track zile simu na kujua gharama iliyotumia, hilo ni jambo muhimu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata humu Tanzania tunaambiwa kwamba kuna watu wana pesa za kutosha (mabilionea) lakini mbona mchango wao hauonekani, mahesabu yao wanatengenezaje? Jambo hilo na lenyewe linatakiwa liangaliwe kwa karibu ili kuwe na equal share katika ulipaji wa kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa 84 na 85 nimpongeze Waziri kwa kufuta baadhi ya kodi kwenye bodi, ni jambo muhimu, tulilitegemea na tunategemea twende zaidi. Suala la industrial sugar (asilimia 10), maana yake sukari hiyo ikiingia inaingia kwenye soko la walaji. Suala hilo pamoja na kwamba sasa tunabadilisha mwelekeo tuangalie usimamizi wake. Iagizwe sukari ambayo itaweza kwenda huko kwenye viwanda lakini huku kwingine tulinde viwanda vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la misamaha ya kodi. Nashauri lisimamiwe kwa ukaribu kwa sababu tunaaamini kabisa iko misamaha yenye tija ambayo inabidi iendelee kutolewa. Hata hivyo, sheria zetu na TIC ziwe aligned, nafikiri mgogoro unakuja hapa kwenye TIC, utafika pale unaambiwa kuna strategic investor sijui kuna nani, maelezo chungu mzima, hayo maelezo yanakinzana na sheria nzima ya ukusanyaji wa kodi. Jambo hili liangaliwe na liwekwe wazi ili isionekane kwamba kuna mtu anaweka sheria zake anazofikiria yeye mwenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukurasa wa 99 kuna suala limezungumziwa kuhusu kudhibiti misamaha ya kodi, kwamba watu walipe baadaye wadai refund lakini tumeshuhudia watu wanakaa kwenye queue kusubiri hiyo refund, pesa haziendi kwa lugha rahisi. Hiyo na yenyewe ina create image mbaya, lakini pia inafunga mitaji ya watu. Kwa sababu mtu anapolipa kodi anategemea refund ili aendelee kufanya biashara yake na mtaji wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lipo jambo lingine ambalo pia inabidi tuliangalie kwa pamoja nalo ni usajili wa bodaboda kuongezewa muda. Ni sawa umeongezewa muda lakini zamani kulikuwa na biashara ya taxi na ilikuwa ni formal business. Biashara ya taxi imekufa, waliochukua nafasi hiyo ni bodaboda, lazima sasa tujue contribution ya bodaboda katika kufidia pengo ambalo taxi imeliacha maana tulikuwa tunakusanya pesa kule. Kwa hiyo, ni jambo ambalo na lenyewe inabidi tutafakari kwa pamoja. Tunatambua kwamba bodaboda tume-create ajira ya kutosha, ni kitu kizuri lakini tuangalie basi mchango wake ukoje. Maana haya mambo tunayozungumza ya maji, umeme wote tutakuja kufaidi kwa pamoja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema tutakopa mikopo ya nje, kuna mikopo ya kibiashara na yenyewe tuiangalie. Kwenye michango Wabunge walisema kwamba tuangalie hii Private Partnership, wawekezaji wanaweza kuja kugharamia baadhi ya miradi ili tuondokane na suala la kukopa kwa wingi mikopo kutoka nje kwa sababu madhara ya mikopo tumeyaona na deni la Taifa linazidi kuwa kubwa. Kwa hiyo, tukisimamia vizuri suala hili tutapiga hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mapendekezo yalitolewa na ni rahisi tu ambayo yangeweza kutusaidia. Tuna wafugaji wetu wa kuku waliomba VAT iondolewe kwenye mashudu ya kutengenezea chakula, lakini naona suala hilo haliangaliwi kabisa lakini nyumbani tumeacha kuku kule wanafugwa. Tulisema suala la kuleta mapinduzi ya uvuvi, tukasema baadhi ya vifaa viondolewe kodi, mfano mafuta yanayotumika kuendeshea boti za uvuvi. Kwenye migodi wanasamehewa kodi kwa nini kwenye uvuvi wasiweze kusamehewa kodi kwenye vifaa vya kuvua samaki kielektroniki? Hayo ni baadhi ya maeneo kama tukiyaangalia kwa uzuri tunaweza tukapiga hatua kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kabisa naamini kabisa kwamba sheria za kodi ni nzuri tu, lakini hazijasimamiwa vya kutosha. Ninaposema hazijasimamiwa vya kutosha nadiriki kusema kwamba mambo ya kisiasa ndiyo yanafanya zisisimamiwe kwa sababu TRA uwezo wa kukusanya kodi na kusimamia wanao, tatizo tukishaanza kuingiza mambo ya siasa wanashindwa kukusanya na kufikia malengo. Ndiyo maana ukifanya trend analysis miaka mitatu, minne iliyopita kuna miaka tumeshindwa kufikia malengo. Kwa nini tumeshindwa kufikia hayo malengo? Ukiwauliza watu wa TRA watakupa sababu na Waziri mhusika akienda kuongea nao watampa sababu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kusisitiza ni nini hapa? Najua TRA wamejipanga vizuri lakini sasa nao wasaidiwe na kusaidiwa kwao ni rahisi zaidi kama sisi tutasimamia sheria. Kama sisi tunavunja sheria nao watashindwa kufikia malengo na baadaye tutawalaumu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii, nafikiri mchango huo utamsaidia Waziri, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia matukio makubwa ambayo siyo ya kawaida; Vituo vya Polisi kutekwa nyara, bunduki kuporwa, mauaji na uporaji wa mabenki na wenzetu Askari wanajitahidi kuhakikisha kwamba wanadhibiti hali hiyo. Ninayo maeneo machache ya kuchangia, lakini moja ni suala la watumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyoona kwenye hotuba zilizotangulia ni kwamba ratio ya Askari ni mmoja kwa 1,071 nchini kwetu hapa, lakini katika nchi zilizoendelea ni mmoja kwa 450. Sasa ni muhimu tukahakikisha kwamba tunafanya jitihada za makusudi kuajiri askari zaidi. Tumeona kwamba kuna wanaoajiriwa, lakini uwepo mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba pengo hilo linazibwa ili kuweza kuwa na usalama wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Jeshi la Polisi limekuwa linafanya kazi, lakini limekuwa na uhaba wa magari. Uhaba wa magari ni tatizo; matukio yanapotokea hawawezi kwenda kwa wakati kwa sababu magari hayapo na machache yaliyopo mengine ni chakavu. Kwa hiyo, ni muhimu ukatengenezwa mapango mkakati kuhakikisha kwamba Polisi wetu wanapata magari ya kutosha na yawepo maeneo yote hasa ya Vijijini kwa sababu matukio hayapo mijini tu na vijijini yapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia liko tatizo la mafuta; Polisi wetu wamefikia hatua sasa ya kuwa ombaomba. Wanaomba mafuta kwa wafadhili mbalimbali, lakini wanapoomba mafuta, wanaomba kwa mhalifu mtarajiwa. Kwa hiyo, mhalifu mtarajiwa atakapofanya uhalifu, Polisi wanakosa nguvu ya kwenda kumkamata kwa sababu anakuwa ni mshirika kwenye utendaji kazi wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wamezungumza suala la BRN (Big Results Now). Suala linalojitokeza hapa ni kwamba mpango umeandaliwa vizuri na ulikuwa uanzie Dar es Salaam, lakini mpango wenyewe haujatengewa fedha za kutosha na hiyo ilikuwa ni pilot study ambayo baadaye ingesambaa kwenye mikoa mingine. Sasa ni muhimu ikaangaliwa namna mradi huu ufanyike na tuweze kuupima ndani ya mwaka huu mmoja na tuone kwamba tutasonga vipi mbele, lakini intent ya mradi huu ilikuwa kudhibiti vitendo vya uhalifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Askari wetu pia wana matatizo ya sare. Askari anatakiwa awe na zaidi ya pair mbili; lakini inapoonekana Askari anakuwa na pair moja tu, tunakoelekea huko Askari watakuwa wanavaa nguo za kiraia kama hatutakuwa makini. Kwa hiyo, ni jambo muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la makazi, limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge waliopita, lakini tukiweka mkakati wa makusudi kwa mwaka huu na kwa miaka inayokuja katika kipindi hiki cha utawala wa Serikali, miaka mitano ya utawala uliopo madarakani, tuna hakika kabisa suala hili litapata ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo habari ya Magereza. Hapa nataka kugusia suala la msongamano. Msongamano huu, kuna namna mbalimbali ambazo zimeshazungumzwa, adhabu mbadala; wengine wafungwe uraiani wafanye kazi za kijamii. Hilo ni jambo jema, lakini inaonekana utekelezaji wake umekuwa ni wa kusuasua sana. Hii ni kwa sababu sheria hizo zilishapita miaka mingi iliyopita, lakini bado hazitekelezwi. Kwa hiyo, nashauri mamlaka zinazohusika zitekeleze kikamilifu ikiwemo ujenzi wa Magereza mapya hasa katika Wilaya mpya ikiwemo Wilaya ya Mkalama. Hilo ni jambo la muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie suala lingine nyeti; mimi niko kwenye Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama; tulitembelea kwenye Gereza la Isanga, kuna eneo ambako wako kuna watu waliohukumiwa hukumu ya kifo. Watu hao na wenyewe wanasongamana; na kwa sababu wamesongamana na utekelezaji wa adhabu hiyo unachukuwa muda mrefu, watu wameshakaa muda mrefu sana kwenye eneo hilo. Kwa hiyo, ni vyema basi kukawepo na tafakari mpya, labda wabadilishiwe kifungo kiwe kifungo cha maisha, lakini waweze kufanya na kazi nyingine na waondoe msongamano huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo, wako watu ambao rufaa zao hazijasikilizwa, wana haki ya kukata rufaa, lakini ma-file yao yako kwenye kanda nyingine. Kwa hiyo, wamekaa hawajui ma-file yao yatakuja lini na wameshakaa kwa muda mrefu. Nashauri zichukuliwe hatua za makusudi kabisa, ma-file hayo ya wananchi yaletwe, rufaa zao zisikilizwe na hukumu itolewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa bado niko kwenye Idara ya Magereza, kumekuwa na changamoto kubwa kwa Askari Magereza kwa sababu dawa haziko za kutosha. Ina maana wafungwa wakiugua Askari Magereza sasa wanachukuwa majukumu la kusaidia kutoa pesa zao mifukoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mahabusu wanapopelekwa kwenye kesi zao Mahakamani, imefikia mahali ambako wanapakiwa kwenye magari ya uraiani; na wenyewe wanatakiwa wawe na magari maalum. Mambo hayo yanatakiwa yaangaliwe kwa ukaribu zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa bado katika Jeshi la Magereza, kuna miradi mbalimbali kama vile miradi ya mifugo na miradi mizuri, tunasema tunataka nchi hii iwe nchi ya viwanda ikiwemo viwanda vya nyama. Tunaamini kabisa miradi hii ikiwekewa mitaji ya kutosha wanaweza wakatoa mchango katika kupeleka malighafi kwenye viwanda vya nyama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Jeshi la Magereza linakabiliwa na uvamizi kwenye maeneo yake. Kwa hiyo, tunaomba Wizara iangalie suala hili, viwanja vyote vya Magereza viweze kupimwa na wawe na hatimiliki ili migogoro na wananchi iweze kumalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, pamoja na mambo yote niliyozungumza, lakini liko jambo moja ambalo naomba Wizara hii kwa kushirikiana na Wizara ya Sheria na Katiba ilifanyie kazi. Lenyewe linahusu mfungwa mmoja ambaye ni binti, yuko Gereza la Isanga hapa, yule amekatwa vidole viwili; kidole cha mkononi na cha mguuni na yuko Magereza. Sasa huo ni unyanyasaji na ukiukaji wa haki za binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba suala hilo Mawaziri husika walichukuwe, walifanyie kazi na walete taarifa. Binti yule ameshakaa muda kidogo kule ndani; akiendelea kukaa ndani ya Magereza na huku amedhulumiwa kiasi hicho, maana yake ni kwamba haki itakuwa haijatendeka. Ni vyema suala hilo lichukuliwe na lifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja mkono na nafikiri ushauri nilioutoa unaweza ukafanyiwa kazi na Wizara. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwa mara ya kwanza katika kikao hiki cha Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya, wanasema mwenye macho haambiwi tazama. Yapo mabadiliko makubwa ambayo Waziri aliahidi alivyoingia kwenye Wizara hii kwamba atafanya mabadiliko makubwa katika Wizara yake na tunayaona. Jambo kubwa zaidi ni kwamba wananchi wanachotarajia ni kuona matokeo chanya, kuona mabadiliko na kupata huduma ambazo zinatolewa na Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kwa makini hotuba ya Waziri imeainisha mikakati mbalimbali na mipango mbalimbali ambayo wanakwenda kutekeleza katika mwaka ujao wa fedha tutakapopitisha bajeti hii. Nami kabla sijasonga mbele zaidi niseme kabisa naunga mkono hotuba ya Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono hotuba ya Waziri, yapo mambo ambayo lazima tuyazungumze kwa sababu sisi ni Wawakilishi wa Wananchi. Japan wanayo management system ya Gemba Kaizen. Gemba Kaizen maana yake unatakiwa uende kwenye eneo la kazi/tukio. Sasa suala la migogoro Wabunge wote tunasimama hapa kuzungumza migogoro ya mipaka. Hilo ni jambo kubwa sana, tunatarajia kabisa kwamba watendaji wa Wizara wafike kwenye mipaka hiyo na wafike kwa haraka na migogoro iweze kutatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilichangia na mwaka huu nimekuwa nikimsumbua Waziri, hata juzi nilikuwa ofisini kwa Waziri na Naibu Waziri nimefika, kumweleza matatizo tuliyonayo wananchi wa Mkalama. Imekuwa ni adha kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lililopita nilimwonesha Waziri picha ya mwananchi aliyekatwa panga kwa sababu ya mgogoro wa ardhi. Hii migogoro ya mipaka inatakiwa ipate mwarobaini wake. Nilimweleza Waziri kwamba tuna mgogoro kati ya Iramoto na Hydom, Eshgesh, Singa ‘A’ na Singa ‘B’, Kikonda na Singida Vijijini, Lukomonyeri na Singida Vijijini, Iguguno na Singida Vijijini, Mpambala na Bukundi ambako ni Simiyu. Sasa migogoro ya mipaka haiishii watu kupigana mapanga tu hata shughuli za maendeleo wananchi sasa wamekuwa wanakwepa kuzifanya maana mtu mwingine anasema yuko Mkalama, mara anasema yuko Hydom, mara anasema yuko Manyara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la mipaka ni muhimu likawekwa wazi na likatatuliwa. Naamini kabisa kwa kasi ya Waziri na Naibu Waziri, jambo hili halitakiwi kuchukua muda na linatakiwa lifanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ofisi zetu hasa za Wakuu wa Wilaya tumezifanya kama Mahakama vile, kwa sababu kila siku watu wako pale wanazungumzia suala la migogoro ya mipaka kati ya Wilaya na Wilaya na kati ya Mkoa na Mkoa, jambo hili tunaomba lipewe kipaumbele. Pia namshukuru Waziri alishaahidi kwamba atalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni upimaji wa Miji na Vijiji. Suala hili na lenyewe ni muhimu sana kwa sababu ziko Halmashauri mpya zimeanzishwa na zilivyoanzishwa kata kadhaa zilitolewa na vijiji vilianzishwa. Hata hivyo, sasa wahusika hawajaenda kuoneshwa mipaka yao. Kwa hiyo, imeanza kuleta migogoro kati ya vijiji na vijiji. Hilo ni tatizo, na lenyewe ni kubwa ambalo linaleta usumbufu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba humu limezungumzwa suala la Hati za Kimila, maeneo mengine ambayo sisi hatujaanza kufika hatua ya juu kwa nini tusipate Hati za Kimila kama wanavyofanya wenzetu wa Kiteto na maeneo mengine, kwa sababu Hati za Kimila inaonekana zinaweza kusaidia kupunguza migogoro hii. Hilo ni jambo muhimu, nawakumbusha tena Wizara, naomba waweze kulisimamia kwa ukaribu kabisa ili tuweze kuishi kwa amani katika Tanzania yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni suala la Baraza la Ardhi. Kwenye hotuba ya Waziri nimeona suala la Baraza la Ardhi na tumeona Halmashauri zingine Mabaraza ya Ardhi yameanzishwa. Hata hivyo, ukiangalia hotuba ya Kamati nanukuu ukurasa wa 18:

“Kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya kuanzisha Mabaraza ya Ardhi katika Wilaya zote nchini.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri wenzetu Kamati wameliangalia hili jambo na wameliona kwa uzito wake na sisi kama Wabunge tunalileta hapa kwa uzito wake. Nieleze masikitiko yangu makubwa. Miezi sita iliyopita Wataalam walikuja Mkalama, wakaja pale wakatuambia masharti yao, wakasema tuwaoneshe jengo, wakaoneshwa jengo wakalikubali lile jengo, lakini toka walivyoondoka hakuna feedback.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kunapokuwa hakuna feedback ndipo uhasama unaanza kati ya wananchi na Wizara pasipo sababu yoyote ile. Kama Rais anatumbua watu, kuna tatizo gani kutumbua hao watu waliokuja miezi sita halafu hawajarudisha feedback? Nafikiri Waziri atachukua hatua na nafikiri wakati wa kuhitimisha atanipa majibu ya kuniridhisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachukulia hiyo kwamba ni dharau, tumedharaulika. Kama mtu anakuja unampa jengo halafu hafanyi kitu chochote ina maana ametudharau na sisi hatuwezi kudharauliwa kwa sababu mimi ni Mbunge wa Jimbo, nawakilisha wananchi wa Mkalama hapa. Kwa hiyo, nasi tuna haki kama ambavyo majimbo mengine yana haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu, sisi ni Watanzania. Wananchi wangu wanapata huduma Baraza la Ardhi Kiomboi ambako ni mbali, kwanza kwenda kule lazima ulipe nauli na ukifika kule labda kesi inaahirishwa au unalala kule. Pia humu ndani kuna akinamama wengi, akinamama wengi wamedhulumiwa ardhi, wajane wamedhulumiwa ardhi, hawapati haki yao. Sasa jambo hilo ni muhimu lazima liangaliwe, kama Baraza linaweza kuanzishwa, kwa nini lisianzishwe watu wapate huduma mahali ambapo ni karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne, nimpongeze Waziri kwa kualika taasisi zake mbalimbali. Tumeona hapa ndani kuna Watumishi Housing, National Housing na mimi nilipata bahati ya kutembelea Watumishi Housing na niliweza kutembelea National Housing, wanafanya kazi kubwa sana. Kwa sababu na wenyewe wako hapa, Wilaya mpya zinazoanzishwa tayari kuna potential ya uwekezaji wa nyumba za wafanyakazi. Kwa hiyo, Wilaya mpya kama Mkalama inahitaji uwekezaji wa namna hiyo iwe National Housing au Watumishi Housing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Mkalama Mjini chumba peke yake choo kwenda nje shilingi 50,000. Sasa kama ni shilingi 50,000 hiyo ni potential market, lakini watumishi wanakaa kwenye substandard house na mtumishi haendi mahali kwa sababu ya mshahara peke yake, mtumishi anakwenda kuangalia na mazingira ya kazi. Kwa hiyo, tunatumaini hizi taaisi zinaweza kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna Mfuko wa Mikopo ya Nyumba kwa watumishi wa Serikali. Mfuko huo ulianzishwa na Sheria ya mwaka 1992. Tunajua umefanya kazi kubwa, ukisoma kwenye bajeti ya Waziri tunauona kama ule Mfuko uko under funded, funding zinazokwenda pale hazitoshi. Tunaomba fund hizo ziweze kuongezwa ili watumishi wengi waweze kupata mikopo na waweze kujenga nyumba pia tuangalie marejesho waliokwishapata urejeshaji wake uko vipi? Ningependa kufahamu Mfuko huu tangu uanzishwe ni watumishi wangapi wamekwishapata hiyo mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine namba sita ni kuhodhi ardhi. Kama alivyosema Waziri hilo jambo ni la kusema hapana, watu wengi wamehodhi ardhi, wananchi wanaongezeka na mtu mwingine anakuwa na ardhi kubwa, kazi yake haitumiii yeye anakodisha watu kulima tu na hiyo iko sana kule Kidarafa, iko sana Mwanga, sasa huo ni unyonyaji, ardhi ya kwetu wewe kazi yako ni kukodisha watu. Nafikiri ni muda muafaka sasa Wizara kuchukua hatua na kuwachukulia hatua wale watu kwa kuwanyang’anya ardhi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la saba ni ardhi versus ongezeko la wananchi. Wizara hii ni Wizara nyeti, Taifa zima linategemea Wizara hii. Nafikiri Wizara inatakiwa ije na strategic plan ya kuonesha ukubwa wa ardhi na ongezeko la watu plus economic activities, mifugo, kilimo, madini, hilo ni jambo muhimu sana. Hata migogoro ambayo ilikuwa inazungumzwa jana kwenye Wizara ya Utalii yote hii inagusa rasilimali ardhi, watu hatujapangwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni jukumu la Wizara hii kuweza kutupanga vizuri na uamuzi unatakiwa utolewe sasa hivi kwa sababu tunapochelewa kutoa uamuzi tunatengeneza bomu ambalo baada ya miaka mingi hatuwezi kulihimili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nafikiri ujumbe utakuwa umefika mahali pake. Tuna imani na Wizara hii na tuna imani na Mheshimiwa Waziri na Naibu wake. Tunatumaini kwamba Tanzania itakuwa Tanzania mpya na watafanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuweza kunipatia nafasi jioni ya leo nami niweze kuchangia kidogo. Ninayo maneno machache sana ya kusema, lakini ni muhimu yakasemwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayofanya na Msaidizi wake Naibu Waziri, wanafanya kazi kubwa sana. Unajua suala la uchumi ni suala mtambuka na ni suala ambalo linahitaji umahiri wa hali ya juu. Kwa hiyo, ukisoma kitabu kimoja kimoja unaweza usipate mwelekezo vizuri, ndiyo maana inabidi usome nyaraka zote halafu ujue tunaelekea wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita zaidi kwenye suala zima la ukusanyaji wa mapato. Jambo la kwanza napenda kuipongeza Serikali kwa kutoa tax amnesty kwa watu ambao wanadaiwa kodi, kwa kuondoa interest na penalty zote zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliposoma kwenye kitabu nikagundua kwamba kutakuwa na tatizo moja, wamesema kwamba ndani ya miezi sita hiyo amnesty ndiyo itaweza kutolewa. Ila nafikiri kwenye miezi sita, kutakuwa na mazungumzo (negotiation), kwa sababu wale wanaotaka kupata huo msamaha inabidi waende kwenye Ofisi za TRA wakazungumze nao, wakubaliane na watakuja kwa nyakati tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pesa kiasi cha shilingi bilioni 500 nafikiri inatarajiwa kukusanywa ndani ya mwaka mzima. Kwa sababu, kama mtu atakuja mwezi wa Nane wakazungumza naye na hawezi kulipa in lumpsum, atalipa kidogo kidogo, ina maana lazima atakwenda mpaka Januari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni muhimu kwa sababu baada ya miezi sita mamlaka husika itakapokwenda kwenye Kamati itakuja kuonekana kwamba hizi pesa hazijakusanywa, kumbe ni suala la administration. Kwa hiyo, suala hilo ni muhimu likaangaliwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la Revenue Forecasting. Nimeangalia hii schedule jinsi mapato yatakavyopatikana, Tax Revenue na Non Tax Revenue, lakini nikawa najiuliza swali moja. Mwaka 2015/2016 nafikiri TRA ndiyo walifikia ile target iliyokuwa imewekwa. Unaposema target, maana yake inakwenda in line na projected plan ambayo inakuwa imeandaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa zile data za kufanyia hizo revenue forecasting zikiwa haziko sahihi sana kwa maana ya sector wise ndizo zina-lead kwenye kufanya ile revunue forecasting ilete majibu ambayo siyo sahihi. Kwa hiyo, jambo hilo inabidi liangaliwe ili tuwe tunawapa malengo sahihi hasa wenzetu wa TRA kwamba waweze kukusanya kulingana na uchumi unavyoruhusu, kwamba uchumi unaruhusu kodi kiasi gani iweze kukusanywa? Kwa hiyo, ni jambo muhimu sana hilo likaangaliwa na wataalam wetu wakaweza kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni suala la mawasiliano (telecommunication). Ukiangalia nchi za jirani, Sekta ya Mawasiliano ina mchango mkubwa sana wa kodi. Sasa hapa kwetu Tanzania sijui kuna tatizo gani kwa sababu bado mchango katika Sekta ya Kodi haujawa wa kutosheleza kwa maoni yangu. Kwa hiyo, nafikiri uko umuhimu wa kufanya utafiti wa kutosha kuona mapato yanavuja wapi, au kwa nini Sekta ya Mawasiliano haijatoa mchango wa kutosha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hesabu ya haraka tu, ukiangalia idadi ya Watanzania walioko na wanaotumia simu; sasa mapato yanayopatikana watu hawatumii simu? Watu wanatumia simu, lakini nafikiri kuna namna ambayo inafanyika ambayo siyo sahihi aidha kwenye kutengeneza hesabu zao, zile expenses zinakuwa nyingi mpaka huko kwenye profit kunaathiri kwenye profit, lakini pia ku-capture data kwa ukamilifu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la EFD, bajeti imesema kwamba watalipa 0%. Nikawa najiuliza swali, sasa hivi kuna suppliers ambao wana stock. Ile stock wanaifanya nini? Kwa sababu stock ilikuwa imelipiwa kodi. Sasa wanafanya nini ili kuweza ku-mitigate au kuweza kufanya kwamba kuwe na fair play kwamba, hawa watakaoingiza zero na hawa ambao walishaleta tunafanya jambo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, hatua kubwa imechukuliwa na TRA na Wizara kwa ujumla kuhakikisha watu wanatumia mashine za EFD na Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amelisemea sana hili suala. Tumekwenda kwenye hii informal sector. Nashauri kama itawezekana, zitafutwe EFD, halafu itafutwe sample group ambapo watu watapewa EFD bure kwenye informal sector waweze kutumia hizo EFD na tuone impact yake itakuwa ni nini? Itakuwa kama ni motisha kuweza kuwafanya watu waone umuhimu wa kutumia EFD, lakini pia watajifunza kufanya mahesabu ya kuweka na kutoa (simple book keeping), litakuwa ni jambo zuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia suala la kodi zilizo kwenye malimbikizo (tax objection) na lenyewe ni suala muhimu sana ambalo Wizara na TRA kwa ujumla wanatakiwa wasimamie waone kwamba zile tax objection zinakuwa cleared. Kwa kutumia window hii ya tax amnest inaweza pia ikasaidia kupunguza zile objections. Kwa hiyo, lazima kuwe na massive campaign ya kuweza kuwaelewesha watu wakajua hili jambo kwa sababu, watakuwa wanarudi nyuma, wanajificha kwa sababu, hawajui faida yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati nzuri nilibahatika kufika SAS, South Africa kule, waliwahi kutoa tax amnest na watu walilipa na walikuwa treated fairly na ilikuwa ni siri yao na kodi ilipatikana. Kwa hiyo, ni jambo muhimu sana kuwe na massive campaign na iwekwe bajeti ya kutosha kwa sababu ndiyo uwekezaji wenyewe. Kwa hiyo, tusibanie pesa mahali tunakoweza kupata pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye lile la non tax revenue tumeona BoT walitoa gawio, NBC na CRDB. Ninachotaka kusema hapa, mashirika yanayosimamiwa na TR sasa imefikia wakati mchango wake uweze kuonekana. Kama mchango wa mashirika hayo ukiweza kuonekana, ndipo tutarudi hata huku kuweza kufikiria kwamba tupunguze baadhi ya viwango vya kodi au tuondoe kodi ambazo ni kero. Natambua kwamba ukisoma bajeti iko very tight kwa sababu vyanzo ni vilevile na lazima uwe na normal flow. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukipunguza Pay As You Earn utaleta madhara makubwa sana kwenye revenue collection. Jambo hilo nalifahamu na ni muhimu tukalifahamu wote tuangalie huku kwa TR anatuletea nini? Pamoja na hivyo, TR naye awekeze zaidi sasa. Kwa sababu, pamoja na mashirika yaliyopo, lakini lazima tuongeze uwekezaji kule ili tuweze kupata pesa za kuweza ku-finance bajeti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nampongeza Mheshimiwa Waziri. Mimi natoka Singida tunalima sana zao la alizeti. Dodoma wanalima alizeti; kwa ku-protect viwanda vya ndani kwa kupandisha kodi, mafuta yatokayo nje ina maana uzalishaji wa ndani utaongezeka. Tatizo kubwa lililopo ukienda hapo Kibaigwa, ukaenda mbele kidogo, ukarudi Singida ukaenda Shelui, utakuta mafuta mengi yako barabarani. Sasa tunafanya utaratibu upi wa kuweza kuwasaidia hao wakulima kwanza kulima wapate mbegu bora, lakini pia kuweza kuyakusanya hayo mafuta yawe katika kiwango kinachokubalika na yaingie kwenye masoko rasmi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, watu hawa wanategemea masoko ya watu wanaopita barabarani na wakati mwingine uratibu wake sasa hata kodi hawalipi pia, lakini tukiweza kutengeneza centres katika maeneo hayo; na ndio hao wafanyabiashara wadogo wadogo ambao tunawazungumza, wajasiriamali, nafikiri mafuta yale ni mengi sana na hata tunaweza tukaya-count. Nina hakika kabisa hatujui kiasi gani cha mafuta kinachozalishwa na wazalishaji wadogo wadogo. Kwa hiyo, jambo hilo ni muhimu likaangaliwa kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya yote yakifanyika kwa ukamilifu wake, nina imani kwamba ile 32 trillion ambayo tunatarajia kuweza kuipata this year, itaweza kupatikana. Pia, mamlaka zinazohusika, wafanyakazi wa TRA basi wafanye kazi kwa juhudi na weledi mkubwa. Tunajua wanafanya kazi kubwa, lakini basi wahakikishe kwamba pesa au kodi inayostahili kukusanywa inapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipenda kusema haya maneno machache, nafikiri yatakuwa yamemsaidia Mheshimiwa Waziri. Nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi ya kuchangia japo kwa dakika moja kwenye Wizara hii. Kwanza nimshukuru kabisa Waziri wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya. Pia nishukuru kwa daraja la Sibiti ambalo limetengewa pesa, tunaamini sasa litakamilika, ndoto hiyo itakuwa imemalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuna sera ya kuunganisha mikoa kwa mikoa kwa hiyo, barabara ya kuunganisha Singida na Simiyu bado hapa kupitia Iguguno, haikuweza kuonekana, kwa hiyo, nilikuwa naomba Waziri atakapojibu aweze kuzungumzia suala hili. Lakini katika ukurasa wa 252, kwenye Kasma 2326, kuna barabara ile ya kutoka Karatu - Mbulu - Haydom - Sibiti River – Lalago mpaka Maswa, hapo katikati inapita…
MWENYEKITI: Ahsante!
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa kunipa nafasi kupitia uchangiaji wa njia ya maandishi ili niweze kuwasilisha mambo machache yanayohusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme hususani katika Jimbo la Iramba Mashariki, Wilaya ya Mkalama na Mkoa wa Singida.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kitabu cha hotuba ya Waziri, ukurasa wa 20 imeelezwa kuwa katika awamu ya III ya REA vijiji vyote ambavyo havikupata umeme vitapatiwa nishati hiyo. Hata hivyo, utekelezaji wa mradi wa REA unaoendelea umeacha maswali mengi kwa Mbunge na wananchi wa Mkalama kwa misingi ifuatayo:-
(i) Vijiji vingi viliachwa yaani havimo katika orodha ya kupata umeme.
(ii) Vijiji vichache vilivyopitiwa na mradi huo nguzo zimepita barabarani na hazijaingia mitaani zilipo huduma za zahanati, shule na huduma zingine za jamii ikiwemo makazi ya wananchi. Mfano ni vijiji vya Kinyangiri, Gumanga, Lambi na Iguguno.
(iii) Vijiji vingi na vikubwa ambavyo baadhi havimo katika mradi huo ni hivi vifuatavyo:-
(a) Kirumi (hospitali na zahanati) Kata ya Matongo;
(b) Mwangeza, Dominiki;
(c) Mwanga, Kidarafa, Kidigida, Msiu;
(d) Kata yote ya Miganga (Miganga, Ipuli)
(e) Mtamba, Kinandili;
(f) Senene, Iguguno Shamba, Mpako;
(g) Yulansoni;
(h) Nyahaa, Mkiwa, Igengu;
(i) Kikhonda, Kinampundu, Mdilika; na
(j) Gumanga kilipo kisima cha maji kilometa 5.
Mheshimiwa Naibu Spika, nina ushauri ufuatao:-
(i) Mradi wa REA upanuliwe ili uweze kufika katika maeneo niliyotaja;
(ii) Nguzo ziongezwe na zifike zilipo huduma muhimu siyo kuishia barabarani;
(iii) Wananchi wanaopitiwa na mradi wa umeme walipwe fidia kwa wakati, mfano wananchi wa Kijiji cha Tamali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwasilisha baadhi ya mambo muhimu ambayo yanatakiwa kupatiwa ufumbuzi wa haraka katika Jimbo la Iramba Mashariki, Wilaya ya Mkalama, Mkoa wa Singida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mkalama imekuwa na changamoto zifuatazo:-
(i) Hatuna Afisa Ardhi Mteule – yupo Afisa Ardhi lakini hajapata uteule, hivyo tunaomba ama tupatiwe Afisa Ardhi Mteule au aliyepo ateuliwe ili shughuli za upimaji ziweze kuanza.
(ii) Wilaya haina Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na tunaomba tupatiwe kwani wananchi wa Mkalama wanapata shida kufuata huduma hiyo Wilaya ya Iramba na kusababisha usumbufu mkubwa wa gharama na muda.
(iii) Migogoro ya mipaka kati ya Wilaya na Wilaya; Mkalama vs Mbulu, upo mgogoro wa mpaka katika Kata ya Mwangeza kijiji cha Iramoto na Kata ya Eshgesh na Mbulu.
(iv) Hali ya usalama ipo mashakani kwa sababu wananchi wa Eshgesh sasa wameamua kujenga shule ndani ya eneo la Wilaya ya Mkalama na watu wa Iramoto hawapo tayari kuona jambo hilo.
(v) Mgogoro wa ardhi Mkalama vs Hanang, jiwe la mpaka kati ya Wilaya hizi mbili limewekwa katikati ya kijiji cha Singa “B” Kata ya Hilbadau, jambo ambalo limezusha mgogoro mkubwa na manung‟uniko kutoka kwa wananchi wa Wilaya ya Mkalama.
(vi) Mkalama vs Singida Vijijini katika eneo la Kata ya Kihonda wananchi wa Singida Vijijini wameamua kujenga shule ndani ya Wilaya ya Mkalama hivyo kuhamisha mpaka bila idhini ya mamlaka husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna migogoro ya ndani ya Wilaya, baadhi ya migogoro hiyo inayohitaji Wizara iingilie ni hii ifuatayo:-
(i) Shamba la Mifugo la Makomoti, mipaka ya shamba hili inadaiwa kupanuliwa/kuongezwa bila idhini ya vijiji husika na baadhi ya wananchi wamejenga ndani ya mipaka mipya na wanalima, hivyo kuanzisha mgogoro mkubwa, vijiji husika ni, Ishenga, Kihonda, Kinyangiri. Tunashauri Wizara iingilie na wataalam wa Wilayani wasihusike kwani wanadaiwa kuwa na maslahi binafsi na eneo hilo.
(ii) Kijiji cha Iramoto kilichopo Kata ya Mwangeza yupo mwekezaji kwa jina la Mr. Afrika ambaye anapewa ekari 700 ambazo ndani yake kuna Kaya 80 hivyo wananchi wanalalamika.
(iii) Kijiji cha Msiu, Kata ya Mwanga yupo mwekezaji anayedaiwa kuwa na haki ya kupewa ekari 200 lakini amehodhi ekari 500 na mahakama imeshindwa kwa makusudi kutoa hati ya mwekezaji huyu kuja kupewa ekari 200 anazostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kupata nafasi ya kuweza kuchangia katika hotuba hii ya Wizara ya Ardhi ambayo ni Wizara nyeti kwa sisi ambao bado tuko nyuma kimaendeleo na ambao tunahitaji huduma ya Wizara hii. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na kama walivyotangulia kusema wenzangu, ule mkoba tulioupata una elimu kubwa sana, tukiutumia ule mkoba vizuri, tukasoma, tunaweza tukapata elimu ya kutosha na ikatusaidia sisi kuweza kuwahudumia wananchi wetu vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama ambavyo nimekuwa nazungumza katika uchangiaji wangu wa awali, wilaya mpya zina changamoto kubwa sana. Wilaya ya Mkalama ambayo ni wilaya mpya hatuna Afisa Ardhi Mteule, ambalo ni jambo muhimu sana, tunamhitaji. Tunaye ambaye amehamishiwa pale lakini hajateuliwa kwa hiyo, namwomba Waziri aidha, tupate mwingine kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI au huyo aliyepo ateuliwe, atakuwa ametutendea haki na atakuwa amewatendea haki wananchi wa Mkalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, huduma za Baraza la Ardhi tunatumia kwa wenzetu wa Iramba ya Magharibi, sisi wilaya yetu ilikatwa kutokea huko, kwa hiyo, tuna shida hatuna Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi. Wananchi wangu wa Mkalama wakitaka kupata huduma hiyo inabidi wasafiri waende Kiomboi walale huko wapate hiyo huduma. Kwa hiyo, tunaomba jambo hilo lifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile wakati jambo hilo linafanyiwa kazi, tunaomba Mheshimiwa Waziri atoe kibali au atoe maelekezo, Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi awe anakuja kufanya mashauri hayo kwenye Wilaya yetu ya Mkalama, inaweza ikatusaidia zaidi, ili kuwapunguzia wananchi gharama. Pia na haki kutendeka kwa sababu, wananchi wanaona wao wamekuwa neglected kwamba hawapati haki kikamilifu wanapokwenda kule na wala hawasikilizwi vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo iko migogoro wamezungumza wenzangu hapa migogoro mingi, lakini katika mazingira ya kawaida na kama machinery za Serikali, organ za Serikali zikiwa zinafanya kazi kawaida haya mambo hayakutakiwa kufika Bungeni wala hayakutakiwa kuzungumziwa hapa, wala hayakutakiwa kufika kwa Mheshimiwa Waziri. Haya mambo tunayozungumza kama Wataalam wangekuwa wamefanya kazi yao vizuri iko migogoro ambayo ingeshamalizwa. Migogoro hii ya mipaka kati ya Wilaya na Wilaya, wakati tunasema tunataka Wilaya au Mkoa upanuke lazima iwekwe miundombinu na wataalam wapelekwe na jambo hilo walimalize na wawashirikishe wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu kuna migogoro mikubwa sana; kuna mgogoro kati ya Wilaya ya Mkalama na Mbulu, kuna mgogoro kati ya Mkalama na Hanang, kuna mgogoro kati ya Mkalama na Singida Vijijini. Jambo hilo limekuwa ni kero kubwa, lakini pia kwa sababu jambo hilo halijafanyiwa kazi kikamilifu unakuta Wilaya moja inakwenda kujenga shule mpakani au inakwenda kujenga kwenye Wilaya nyingine. Sasa imeleta mkanganyiko mkubwa sana tunaomba kabisa Mheshimiwa Waziri na Naibu wako tunawaamini jambo hilo lifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia iko migogoro ya ndani ya Wilaya nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na timu yake, wameleta orodha ya migogoro lakini swali nililokuwa najiuliza kuna watu walipewa kazi hii ya kubainisha migogoro mbona migogoro mingine haikuingia? Tafsiri yake ni nini, inanipa picha kwamba, sasa jambo hili linatakiwa Mheshimiwa Waziri mwenyewe avae viatu aingie vitani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyokuwa tunapiga kampeni, unakumbuka mgombea Urais na Makamu wake walikwenda majimboni, mwingine kushoto mwingine kulia, wanaweza kabisa mwingine akaenda kushoto mwingine kulia na wataalam wao jambo hili katika kipindi hiki likamalizika, kwa maana ya Tanzania nzima watu wenye migogoro. Kwa sababu, mambo haya hayahitaji rocket science, ni mambo ya kiutawala, yanahitaji wafike pale penye mgogoro na wawaelimishe watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko shamba la mifugo linaitwa Makomit, linaleta mgogoro sana katika vijiji vitatu; Kuna Kijiji cha Ishenga, Kijiji cha Kinyangiri na Kijiji cha Kikhonda na nasema ni mgogoro kwa sababu Mbunge siku zote anapita barabara hiyo. Kama walivyosema Wabunge wengine waliopita hapa ni kwamba, viongozi waliokuwepo si Wakuu wa Wilaya ama Wakurugenzi, wanakuja wanafanya kazi, wanafanya mikutano ya ujirani mwema, wanahama. Wanapohama mgogoro wanauacha palepale, anapokuja mtu mpya au kiongozi mpya, mtaalam mpya anaanza jambo hilo upya, sasa jambo hilo limekuwa gumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, nafikiri wale watu hawana muscles za kutatua hii migogoro, sasa muscles hizo ziko Wizarani, Wizara tunaomba itume watu makini waimalize hii migogoro na sisi tuwe Wabunge kwa amani kwa sababu, moja ya changamoto ambayo tunapata ni jinsi tutakavyoimaliza hiyo migogoro. Tusipoimaliza inakuwa ni changamoto kubwa sana, hilo ni jambo la muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, wamezungumza wenzangu suala la sehemu zinaitwa business centres, hizi business centres zinakua kwa haraka sana, maeneo hayo yaje yapimwe, mipango miji iwekwe kwa sababu, baada ya muda nako vijijini kutakuwa na squatters kama zilivyo Dar-es-Salaam na maeneo mengine, lakini ni jambo ambalo linaweza likafanyiwa kazi mara moja na lenyewe likamalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza Hati za Kimila; Hati za Kimila zitolewe turasimishe hayo maeneo ili hao ndugu zetu, wananchi wetu tunaowaongoza waweze kukopesheka, lakini pia, waweze kutambuliwa na tuweze kumaliza migogoro midogo midogo ambayo inazunguka mazingira yetu. Mambo haya yanawezekana kabisa kwa makabrasha mliyotupa hapa, inaonekana Wizara ya Ardhi ina wataalam wa kutosha na tuna imani hiyo na katika Serikali hii ya Awamu ya Tano tunataka tuone hayo mabadiliko ili na sisi tuwe tunatembea vifua mbele tujue migogoro hiyo imemalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, “yuko mtani wangu mmoja anaitwa Mheshimiwa Waitara” anafikiri Dar-es-Salaam anakaa peke yake. Mimi nakaa Dar-es-Salaam vilevile na nakaa Kimara, eneo la Kimara lirasimishwe watu wapewe maelekezo maeneo yao yatambuliwe. Maeneo yao yakitambuliwa labda wanatakiwa kuhama waambiwe kwa sababu, huwa linakuja suala watu tunaanza kubomolewa nyumba zetu kule na mimi nina nyumba kule tunaanza kuleta mgogoro. Kwa hiyo, tunaomba jambo hili na lenyewe liweze kupatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini uko mgogoro mwingine kati ya sisi na Simiyu, ule Mto Sibiti unahama kwa hiyo, mto unapohama na mpaka unahama vilevile. Kwa hiyo, ni muhimu wananchi wetu wakaelekezwa mpaka uko wapi na pande zote mbili hizo zikashirikishwa na sisi kama Wabunge wa maeneo yote niliyoyataja hapa tuweze kushirikishwa ili tuweze kukaa kwa amani na tuweze kuwatumikia wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba na lenyewe tunalialika waje Mkalama, wilaya ile ni mpya kuna wafanyakazi wengi, zaidi ya wafanyakazi 100, hawana mahali pa kuishi. Mkija mkijenga kule na eneo tutawapatia, mtakuwa mmetusaidia sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, hizi nyumba zinazojengwa zinazouzwa wanazoziita za gharama nafuu ziangaliwe, ziko nyumba zimejengwa pale Singida zimebananabanana, unajua utamaduni wa mikoani na mjini uko tofauti, designing ibadilike; halafu thamani ya milioni 40 au milioni 50 ionekane, kwamba hii ni milioni 40 na hii ni milioni 50. Bado opportunity iko kubwa wanaweza wakapanuka zaidi na Shirika letu la Nyumba likaweza kusaidia zaidi Taifa letu hili na watu wanaona kazi ambayo wanaifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ujumbe wangu umefika, maana tunasema ni muda wa kazi tu, hatuna mambo mengi sana hapa, unafikisha hoja zako unatulia. Naunga mkono hoja, asanteni.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi nami niweze kuchangia hotuba hii. Nashukuru sana kwa kunipa hizo dakika tano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Waziri kwa Hotuba yenye data nyingi ambazo data hizo ukizipitia kila mtu anajua yuko katika nafasi ipi, lakini kwa ujumla napenda kusema kwamba, pesa za maji zinakuja nyingi, wafadhili wako wengi, lakini mgawanyo wake unaleta mashaka kwa sababu, nguvu kubwa inaelekezwa mijini. Ndiyo maana watu wanasema kuwe na Wakala wa Maji Vijijini. Vile vile asilimia za maji ambazo zinatolewa vijijini haziko sahihi! Niko tayari tufuatane na Waziri, tufanye kwenye Jimbo langu kama liwe Jimbo la Mfano, tuone asilimia ya wananchi wangapi wanapata maji, asilimia 72 haijafika hiyo na haitafikia kwa uharaka wa kiasi hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, suala la maji tuangalie vyanzo vya maji. Mkoa wa Singida ni mkoa kame, kama ni mkoa kame vyanzo vyake ni vya visima, hatuna mito, ingawaje lazima tufikirie mbali; wenzetu wanakunywa maji ya Mto Nile, bomba la mafuta linatoka Uganda mpaka linafika Tanga, gesi imesafirishwa kutoka Mtwara mpaka kwenda Dar-es-Salaam, equally maji ya Ziwa Viktoria yanaweza kusafirishwa yakafika Singida na yakafika Mkalama. Kwa hiyo, ni jambo ambalo linatakiwa tukae chini tuweze kulitafakari tuone tutafanya vipi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 134 kuna pesa zimetengwa. Ukiangalia pesa za Mkoa wa Singida ni asilimia mbili nukta mbili katika bajeti yote; ukiangalia zile column unasikitika kuna bilioni tatu, bilioni nne, unakwenda wengine milioni 600, kigezo kipi kilitumika? Ukiangalia Mkalama milioni 600 watu 188,000, vijiji 80! Hayo maji yanatosha? Hayo maji hayawezi kutosha! Naamini kabisa, hakuna Mtaalam aliyefika kule! Katika hilo naondoka hapa nikiwa nimeshawishika hivyo!
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini iko miradi ya maji ambayo ilikuwa imeanza kutekelezwa, Iguguno, kuna wakazi 10,000! Mradi huo umeshindikana kukamilika! Mtamba, mradi huo umeshindwa kukamilika! Kidarafa umeshindikana! Kikonda umeshindikana! Watu wamechoka kusikia maneno, watu wanataka kunywa maji, hilo ndiyo jambo la muhimu! Wanaosimamia wanafanya kazi gani? Mheshimiwa Waziri naomba atakapojibu hapa, watu hao awafahamishe kwamba, hiyo miradi itakamilika lini? Tumezungumza huko kwenye ma-corridor nikamweleza, kuna mafundi wanazungukazunguka, lakini hakuna kinachoendelea!
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kuna maeneo kame kama vile Mpambala, Nyahaa, Endasaki, Mwangeza, Iguguno, tulitarajia kuwe na mabwawa. Hata kama bwawa moja kwa mwaka kwa miaka mitano tutapata mabwawa matano, lakini hatupo, tumeachwa watoto yatima. Jambo hilo liangaliwe na maeneo mengine kame ya Dodoma yaangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini scheme za umwagiliaji, imezungumzwa scheme ya msingi, huu ushirikishwaji mimi sielewi unaanzia wapi? Ziko scheme ambazo zimekuwa abandoned, kama Mwangeza iko scheme ya umwagiliaji na kulikuwa na miundombinu pale, lakini haijatokea humu! Kwa hiyo, inaonekana hawa Wataalam wanakwenda kwa maslahi yao binafsi.
Ndugu zangu ni vema tukawa tunafundishana humu ndani kwa ndani tuangalie mifano ya Wizara nyingine zinafanyaje? Ukichukua mwenzako amefanya nini inaweza ikaleta tija, tumeona Nishati mambo ya REA! Tumeona REA inasonga mbele! Kwa nini na sisi tusiwe na mfumo kama wa REA kuhusu maji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweka hivyo na tukaweka muda kwamba, kwa miaka mitano au miaka 10, tutakuwa tumepiga hatua na jambo la maji litakuwa historia ikiwepo watu kupata maji salama. Hata hivyo, ukisoma ukurasa wa 109 kuna deni la shilingi bilioni 212; lazima tuone pesa zimetumika wapi? Ifanyike auditing, kama hiyo miradi inayozungumzwa ya Iguguno watu wanadai madeni na kwenye majimbo mengine ina maana hizi pesa hazikutumika! Hizi pesa tunashawishika kuwa watu wamegawana! Wametengeneza vitu ambavyo ni sub-standard miradi imeshindwa kukamilika, ifanyike auditing tuweze kujua kabla hamjalipa hizo pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nizungumzie maji mijini, pale Dar-es-Salaam; hawa DAWASCO wanafanya biashara wanawaonea wateja! Mimi kama Mbunge wamenikatia maji nyumbani kwangu wananiambia nilipe laki tisa, nalipa kwa sababu mimi Mbunge! Mtu wa kawaida atapata wapi laki tisa? Wanafunga maji watapata wapi? Pale DAWASCO Kimara yale ni majipu matupu yale! Sasa wananchi wa Dar-es-Salaam mlaji nae aweze kulindwa. Mheshimiwa Waziri naomba jambo hili alichukulie kwa umakini na kwenye mamlaka nyingine za maji ili watu waweze kupata maji kwa wanachotumia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji ni suala la muhimu. Tunaomba sisi ambao hatuna mito inayotiririka kwa mwaka mzima, tupewe kipaumbele kwa maana hiyo, hata bajeti iweze kuongezeka. Unategemea viwanda vitajengwaje katika wilaya kama hizo ambako maji hayapo? Unategemea wananchi watarudi vipi vijijini kama hawapati huduma ya maji? Unajua watu mijini wanafuata umeme, wanafuata maji, wanafuata barabara na vitu vya namna hiyo! Kama tunataka wananchi wetu, miji yetu ipumue, watu warudi vijijini, lazima miundombinu na huduma hizo muhimu ziweze kupatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi hiyo. Nafikiri ujumbe wangu umefika vizuri kabisa kwa Waziri. Naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia. Ninayo mambo manne na mambo yenyewe ni mafupi mafupi tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, Sera ya Mambo Nje inabidi ifanyiwe marekebisho, tunajua ni ya mwaka 2001 kwa sababu sera ndiyo inatoa mwelekeo, tunakoelekea, inaweka priority zetu, hilo ni jambo la muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, tunasema mtengamano, fursa zilizopo, tumepata machapisho mengi, lakini ni jambo la ajabu hata sisi Wabunge tunauliza, hatujaujua sawasawa huu mtangamano. Sasa ni wakati muafaka wenzetu hawa wakachukuwa hatua za makusudi kuwaelimisha jamii inayozunguka, watu walioko mipakani waelimishwe na sisi Wabunge tuelimishwe ili tuweze kutumia fursa hizo. Kwa sababu fursa hizi zinafahamika tu kwa Wabunge wa Afrika Mashariki, zinafahamika na baadhi ya watu tu, lakini Mwananchi wa kawaida; katika nchi yetu tuna utaratibu wa utawala, tuna wenyeviti wa vitongoji, tuna wenyeviti wa vijiji wanaweza wakatumiwa hasa mipakani kuhakikisha kwamba, elimu hii inawafikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la Diaspora limezungumziwa sana, watu walioko huko. Mimi najua kwamba, iko diaspora, kuna forum ya diaspora na huwa wanakusanyika wanatambuana katika nchi mbalimbali wanazoishi licha ya mchango wanaopaswa kuuleta huku kwetu, lakini pia wao wanatakiwa kutambuana. Ni ukweli usiopingika kwamba watu wengi wamekwenda kule wamejilipua, hawatambuliki katika Balozi zetu, kama hautambuliki katika Balozi zetu zilizoko huko, utapataje huduma hiyo? Kwa hiyo, ni wakati muafaka sasa waliojificha huko watoe taarifa kwenye Balozi ili waweze kupata huduma zinazohitajika badala ya kuendelea kulalamika tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine limezungumziwa hapa, suala la Rais kusafiri nje ya nchi; kuna leadership style, leadership style ni muhimu, kiongozi anaweza akawa anasafiri nje na ikawa sawa lakini yuko kiongozi mwingine, yuko anafanya strategic planning nyumbani. maadamu nchi inakwenda, inasonga mbele na tunaona matokeo, kama tunaona matokeo hana sababu ya kusafiri. Atasafiri itakapo kuwa ni lazima, huo ni utaratibu wa uendeshaji wa nchi yake. Hata wenzetu hawa wakipata nchi watapanga utaratibu wao wa kuendesha nchi, huu ndiyo utaratibu unaoonekana ni utaratibu bora. Kwa hiyo, inabidi tuheshimu utaratibu huo, tuone nchi inaendeshwaje na sisi Wabunge hapa tushauri ili tuweze kuona kwamba tunatoa mchango katika uendeshaji wa nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mabalozi; suala la Balozi kuzuiwa, limesemwa wanazuiwa kuwasiliana na maeneo mbalimbali, amesama msemaji wao mmoja. Uko utaratibu, hapa ni Tanzania na hapa ni kwetu na sisi ndiyo Watanzania. Balozi hawezi kuja hapa akafanya mambo anavyotaka yeye, lazima Balozi akija hapa anakuwa Monitored na asipofuata taratibu hizo tunamchukulia hatua na tunaweza kumrudisha alikotoka. Na hii imeshaonekana ni practice World Wide, inafanyika na sisi hatuwezi kwenda tofauti na hivyo. Lazima tuilinde nchi yetu, lazima tuwe na uchungu wa nchi yetu, tuweze kuona kwamba Taifa letu linakuwa salama na hao Mabalozi wanafanya kazi walizotumwa sio wanafanya kazi, ambazo wanafikiria wao kichwani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ya kwangu yalikuwa ni hayo machache tu, asante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii kuipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa utekelezaji na usimamiaji mzuri wa mipango ya Serikali iliyoandaliwa kwa kuzingatia Ilani ya CCM. Hata hivyo napenda kuchangia katika maeneo yafuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama; Ofisi ya Waziri Mkuu itambue kuwa Wilaya ya Mkalama ni moja kati ya Wilaya mpya na huduma za mahakama zinazopatikana katika Wilaya ya Iramba (Kiomboi) na hivyo kusababisha usumbufu mkubwa na haki kupotea kwa wananchi wa
Wilaya hii. Ninaomba katika bajeti ya mwaka 2017/18 Wilaya ya Mkalama ijengewe Mahakama ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkalama wanajihusisha na kilimo kinachotegemea mvua za msimu lakini kwa bahati mbaya mvua hizo zimenyesha chini ya wastani katika msimu wa mwaka 2016/2017 unaomalizika sasa na ofisi ya Waziri Mkuu imefanya tathimini na kubaini
kwamba Halmashauri 55 zimeathirika na ukame. Hivyo napenda Ofisi ya Waziri Mkuu itambue na kuingiza Wilaya ya Mkalama katika Halmashauri zilizoathirika na ukame kwani kata zifuatazo mvua haijanyesha, Mpambala, Mwangeza, Gemenga na Mafongo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya madini inatoa mwongozo wa usimamiaji vizuri wa sekta hii lakini uzoefu unaonyesha kuwa uratibu wa sekta hii ikiwemo utaratibu wa utoaji leseni hauendani na sera iliyopo mfano. Leseni za kuchimba madini ya gypsum katika eneo la Dominiku -
Mkalama bila wananchi kuhusishwa na hivyo kuzua migogoro kati ya wananchi na waliopewa leseni. Tunashauri Serikali ichukue hatua na kufuta leseni hizo au kuhakikisha wananchi wanapata fidia stahiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migogoro ya mipaka na ardhi napenda kuweka bayana kuwa migogoro ya mipaka kati ya Mkoa na Mkoa na Wilaya kwa Wilaya haijapatiwa ufumbuzi ama kama zipo juhudi basi zinaenda kwa mwendo wa kinyonga yaani polepole. Tangu niingie
Bungeni nimetoa taarifa za kuwepo mgogoro katika maeneo yafuatayo; mgogoro wa Singida - Manyara na Singida – Simiyu. Migogoro hii ya mipaka inasababisha migogoro na mapigano kati ya Wilaya zifuatazo; Mkalama - Mbulu, Eshijeshi - Iranoto, Mkalama - Mbulu, Singida A – Singida B, Mkalama - Singida Vijijini, Mkarama - Iramba na Mkalama - Nyahaa – Simiyu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume iliyoundwa naamini haina taarifa hizi na wapo wananchi wameumizwa kwa mapanga. Nashauri suala hili litolewe maagizo maalum lishughulikiwe.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nishukuru kwa kunipatia nafasi
ya kuweza kuchangia katika Wizara hizi mbili. Nizipongeze Wizara zote hizi mbili na Kamati kwa
kazi kubwa zilizofanyika kwa ujumla wake na tunaweza kuchangia hapa kwa sababu kuna kazi
ambayo imefanyika na tunaiona.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la REA. Suala la REA kazi kubwa imefanyika,
lakini bado tunaomba Wizara ifuatilie kwa karibu. Nasema ifuatilie kwa karibu kwa sababu REA II
ambako umepita, umeme umepita barabarani tu. Nguzo zimeingia kidogo sana na jambo hili
tumekuwa tukilizungumza kwa nyakati zote. Kwa hiyo, hao wakandarasi wanapofanya kazi
inabidi wafuatiliwe. Ukienda sehemu kama za Kinyangiri na Ngalakala, maeneo yote yale
umeme haujaingia sana ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine katika Wizara hiyo nizungumzie suala la
madini. Sisi kule Mkalama tumepata madini ya gypsum na madini mengine ya shaba yapo,
lakini kinachotokea ni kwamba watu wanakuja na leseni wanaanza kuchimba madini bila kuwa
na utaratibu. Tunaposema utaratibu, maana yake waje, waonane na vijiji husika, wakionana na
vijiji husika basi kunakuwa na utaratibu wa kuanza kufanya kazi hiyo bila manung‟uniko. Sasa
hao watu wanaopata leseni wanakuja huku wanatuletea migogoro na Maafisa Madini wa
Mkoa wao wanawapa barua tu wale watu wanakuja lakini lazima uweke utaratibu mzuri
kurekebisha jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikienda kwenye suala zima la barabara, kwanza
kwenye ukurasa wa 53 wamesema kuna barabara mikoa ambayo haijaunganishwa kwa lami
lakini sikusikia Simiyu wala Singida. Nafikiri ilikuwa ni mfano tu sasa tusiwe tunasahaulika Simiyu na
Singida, ni jambo la muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine; suala la alama za barabarani. Sasa hivi
kumekuwa na mgogoro mkubwa, alama nyingi zimepelekwa chuma chakavu. Mimi nafikiri
kama Kamati ilivyopendekeza sheria itungwe, lakini pia hatua zichukuliwe, kuwa na nguzo za
saruji labda inaweza ikasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spik ukienda Mlima Saranda pale kila siku wanafanya ukarabati
kwenye Mlima Saranda, zile kingo zinagongwa kila siku, ukarabati huo una gharama kubwa.
Sasa hakuna njia mbadala au kuna tatizo gani pale? Ziwekwe kamera tuone labda watu
wanakuja kwa mwendokasi ndiyo maana ajali zinakuwa nyingi, ukarabati wa zile kingo naamini
kabisa unagharimu pesa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya barabara inayogharimiwa na Serikali yakiwemo
madaraja, pia likiwemo Daraja la Sibiti. Miradi hiyo imekuwa inachelewa kwasababu pesa za
ndani haziji kwa wakati na jambo hilo limezungumzwa na Kamati. Serikali inabidi ione athari
zake, kwamba gharama za mradi zinaongezeka ikiwepo gharama wakandarasi na wale
washauri waelekezi, limekuwa ni jambo kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wale wataalam washauri wamekuwa na tabia ya
kuegemea upande wa mkandarasi Kamati zikienda. Kwa nini hawawi upande wa Serikali ili
kuweza kuona ubora wa miradi? Jambo hilo ni muhimu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala lingine la barabara TANROADS, watu wanajenga
kwenye maeneo...
(Hapa kengele ilia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuipongeza Wizara ya Katiba na Sheria kwa kazi nzuri inayofanywa. Pamoja na kuwepo changamoto ya umuhimu wa kuboresha baadhi ya sheria ambazo ama zimepitwa na wakati au zinahitaji kuweka mkazo/udhibiti katika baadhi ya maeneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma hotuba hii kikamilifu na kubaini kuwa ahadi iliyotolewa Bungeni na Waziri mtangulizi kuhusu Wilaya mpya ya Mkalama kutokuwa na Mahakama ya Wilaya ilihali wananchi wakiifuata haki Wilaya ya Iramba Magharibi. Wakati jibu likitolewa katika swali la msingi lililoulizwa na Mbunge wa Iramba Mashariki Mheshimiwa Allan Kiula iliahidiwa kuwa bajeti ya Wizara ya mwaka wa fedha 2017/2018 itaweka/itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Mkalama lakini sijaona utekelezaji wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara itenge fedha katika bajeti hii ili kuwasaidia wananchi wa Mkalama ambao wamewekwa wakihangaika kupata haki katika Wilaya nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nimpongeze Waziri na watendaji wa Wizara kwa kazi inayofanyika sasa. Pongezi hizo zinatokana na ukweli kuona Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameonesha njia na uongozi mahiri wenye kulenga kuibadili Tanzania na kupiga hatua za haraka katika maendeleo. Yapo mambo mengi yamefanyika ikiwemo ujenzi wa reli ya standard gauge, kufufua ATC, kutenga asilimia 40 ya mapato na kuelekeza katika shughuli/miradi ya maendeleo. Pamoja na pongezi hizo, yapo maeneo muhimu ya kuchangia kama ifuatavyo:-
(i) Daraja la Sibiti linalojengwa sasa na shilingi 3.5 bilioni zimetengwa lakini barabara hiyo yenye daraja linalounganisha Mkoa wa Simiyu na Singida lakini katika bajeti hiyo ni lini upembuzi yakinifu utafanyika?
(ii) Wilaya ya Mkalama ni mpya na haina hata kilomita moja ya lami na zipo shughuli nyingi za kiuchumi, tunaomba Wizara itenge fedha za ujenzi wa kilomita 30 za lami kutoka Iguguno –Ndugahi yalipo Makao Makuu ya Wilaya.
(iii) Bado wananchi wa Mkalama wanapata shida ya mawasiliano kutokana na kutokuwepo minara ya kutosha. Tunaomba Wizara iweke mikakati ya kuhamasisha makampuni ya simu kuweka minara hasa katika Kata za Kinyampanda, Mwangeza, Ibaga, Mpambala, Msingi na Kinyangiri.
(iv) Zipo barabara ambazo hazihudumiwi na TANROAD wala Halmashauri pamoja na kuwa maeneo husika yana wakazi wengi pia ni maeneo yenye uzalishaji mkubwa mazao hasa mahindi na alizeti. Hivyo, naomba Wizara ichukue jukumu hili kwa kufungua barabara husika ya Msingi – Yulansoni – Lyelembo -Kitumbili (kilomita 25).
(v) Ipo barabara ambayo inaunganisha mikoa miwili kupitia Wilaya ya Mholame nayo tunaomba itengewe fedha, upembuzi yakinifu ufanyike. Ni barabara ya Haydom - Kidasafa – Nkungi - Ilongero - Singida (kilomita 93.4).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi kwa kuweza kupata nafasi kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Cha kwanza kabisa naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri, pili naunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli za kuiongoza nchi hii kwa umakini kabisa na kwa uhodari mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, nilitaka kuweka jambo moja sawa kwamba bajeti inakua, bajeti haiwezi kusimama hapo hapo, bajeti lazima ikue. Ili bajeti iweze kukua kuna mikakati ambayo inakua imewekwa. Kwa mfano tumeweka mazingira mazuri ya kujenga viwanda, na viwanda vinajengwa na wadau mbalimbali Serikali haijengi viwanda. Vilevile mmeona tunatengeneza miundombinu, miundombinu ikikaa sawa ina uhusiano wa moja kwa moja. Tumegusa suala la kilimo, kilimo pia kitasaidia kuleta malighafi katika viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie suala lingine la kusema kwamba CCM itaondoka madarakani, lakini siku chache zilizopita TWAWEZA wametoa takwimu hapa, wameonesha nani anapanda, nani anashuka. Mimi sipendi kuingia huko lakini TWAWEZA wameweza kutuonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia suala zima la bajeti sasa katika mchango wangu, bajeti ni shilingi trilioni 31, lakini kodi ni shilingi milioni 17 na tax revenue shilingi trilioni mbili na madeni ni shilingi trilioni 11 ndipo tunafika kwenye shilingi trilioni 31 maana yake nini? maana yake ni lazima tuangalie vyanzo vipya vya mapato. Na vyanzo vipywa vya mapato vya haraka haraka lazima informal sector, World Development Report ya mwaka 2017 inazungumza kwamba katika nchi zinazoendelea, informal sector ina-constitute karibu asilimia 40; sasa lazima tuangalie hiyo informal sector tutaileta vipi kwenye net ya kulipa kodi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo machache ambayo pia yanatakiwa yaangaliwe, consultancy. Watu wanafanya consultancy lakini hawalipi kodi, lakini kuna watu wanafanya kazi mbili/mbili hawalipi kodi lakini pia Rais amesema mikataba itakuja ya madini, mikataba ya madini ikija itaongeza kipato, na hiyo inajibu hoja ya kusema hatukuweza kukusanya vya kutosha, hatuku-perform vizuri. Pesa zinakuja, pesa zikija tutaweza kuigharamia bajeti yetu bila tatizo lolote lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo lazima sote na Waziri atambue kwamba tumeweka mpango na lazima pesa zipatikane, kwa hiyo, pesa zitapatikana kwa kuweka mikakati mizuri na pesa zikipatikana mimi nina uhakika kabisa hata Jimbo langu la Mkalama Daraja la Sibiti litakamilika, barabara zitakamilika, huduma ya afya itakuwa sawa na maji watu watakunywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la motor vehicle. Tumeondoa motor vehicle, tumeweka utaratibu huo mzuri wa shilingi 40. Hiyo shilingi 40 tupige hesabu tuone kwamba tulitakiwa tukusanye pesa ngapi kama tusingeondoa motor vehicle. Kwa hiyo pesa iliyozidi ambayo mimi nimepiga hesabu hiyo pesa imezidi imepelekwe kwenye maji iwe refenced, ichangie kwenye mfuko wa maji itakuwa ni jambo zuri.

Niende kwenye suala la madini. Tumezungumzia suala la gypsum nazungumza suala la gypsum kwa sababu kule kwangu Dominiki gypsum ipo. Nashukuru Serikali kwa kuona viwanda vya ndani kutumia gypsum ya hapa kwetu, lakini basi uwekwe utaratibu mzuri wananchi wawezeshwe. Hiyo gypsum mimi niliangalia haina utaalam sana wa kuchimba, kwa hiyo, kama Wizara ya Madini na Nishati itawawezesha wananchi kuweza kuchimba hiyo gypsum wenyewe na masoko ambayo tunayajua wananchi watanufaika. Pia wale maofisa wa madini wanatoa leseni tu wananchi wanakwenda kuondolewa bila utaratibu wowote, hilo jambo liangaliwe na huko wananchi wanaweza kunufaika na madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao chini ya tani moja. Tumesema kwamba mazao chini ya tani moja yasilipiwe ushuru wowote. Hapa yako mambo mawili, kwanza tunaipongeza Serikali kwa hatua hiyo lakini tutambue kwamba wako wafanyabiashara wajanja, walanguzi ambao wanaweza wakatumia mwanya huo kupoteza mapato hayo. Sasa viwekwe vituo vya kuuzia mazao, kwa hiyo, Halmashauri wapewe leseni za kununua mazao kwenye vituo maalum tusiruhusu walanguzi kuingia kwa wananchi na yenyewe itakuwa ni jambo litakalosaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tujue kwamba sasa Halmashauri zitapoteza mapato, kwa hiyo tukadirie tuone kwamba mapato yatapotea kiasi gani na tuone hizi Halmashauri zitafidiwa kiasi gani. Kwa mfano, sisi Mkalama zile own source kubwa zinategemea hizi kodi……..

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza Wizara kupitia Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ya kusimamia Wizara hii. Natambua Waziri alifika katika Jimbo langu la Iramba ya Mashariki na kuona tatizo la maji na jinsi watu wanavyohangaika, hii ni tofauti na mifugo. Ninashauri yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ukaguzi kwa mradi wa uchimbaji visima katika vijiji kumi pesa ambazo zilitolewa na Serikali lakini baadhi ya visima havina maji ya kutosha na pesa zimelipwa. Serikali ione namna ya kujenga na kutoa fedha kwa ajili ya mradi huo wa visima kumi. Pia Serikali ione namna ya kusaidia Wilaya kame kupata malambo na mabwawa ikiwemo Mkalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Makao Makuu ya Wilaya ya Mkalama ni Nduguti, mji ambao hauna maji. Naomba Wizara ione namna ya kuanzisha mradi maalum katika Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetoa shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya Kinyambuli, ni muhimu mradi wa maji ukapelekwa kwenye kituo hiki cha afya.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami kuweza kupata nafasi ya kuchangia katika mawasilisho ambayo yamewasilishwa na Wenyeviti wa Kamati. Ningependa kujikita kwenye wasilisho la Kamati ya PAC, yapo mambo ambayo yanabidi yatolewe uamuzi na Bunge ili yajadiliwe kwa kina ili kuweza kuweka mambo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia suala la Mlimani City, Mlimani City limeelezwa kwenye taarifa ya PAC na tumeweza kuona ambavyo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hakinufaiki Mkataba wa Mlimani City. Ukisoma kwa kituo, paragraph hiyo, utaona jinsi mwekezaji alipokuja na jinsi mtaji wake alivyoutoa na baadaye akatengeneza madeni, akaenda TIC akaweza kunufaika na msamaha wa uwekezaji.

Mheshimiwa mwenyekiti, pia tumeona uendelezaji, tulitembelea Mlimani City pale katika maeneo ambayo yanatakiwa yaendelezwe, kimkataba kama walivyokubaliana hayaendelezwi, kuna hoteli ya nyota tatu haijajengwa, lakini pia kuna botanic garden haijafanyiwa kazi na ukiangalia kwenye maelezo yao kuna mahali wale watu wanagawana dividend, kwa maana kuwa mradi huo una faida, lakini pia hawalipi kodi stahiki kama walivyokubaliana kwenye mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya mahojiano na wenzetu wa Chuo Kikuu, ikaonekana wanaendelea na mazungumzo, lakini mazungumzo hayo wanayofanya, eneo lolote lile ambalo, lina manufaa kwa Chuo Kikuu yule mwekezaji, halitaki, isipokuwa anataka maeneo ambayo wao wanaona kwamba wanaweza kunufaika nayo, ndipo hapo mabadiliko yafanyike, wa-review ule mkataba, ukiwemo muda wa mkataba ambao ni muda mrefu sana, lakini pia wameendeleza wamefanya extension pale, hiyo extension iliyofanyika, imefanyika haikuwemo kwenye mkataba na wameendeleza maeneo ambayo wanapata pesa. Kwa hiyo suala zima la Mlimani City, inabidi liangaliwe kwa macho mawili na Bunge hili lazima liazimie, mkataba huo upitiwe upya na TIC watoe maelezo ya kutosha ili tuweze kuona chuo kikuu kinanufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo zima la ukopeshaji wa matrekta Suma JKT. Bunge lililopita tulizungumza kwamba bado yapo madeni makubwa watu hawajalipa matrekta, kwa hiyo, matrekta yanakuwa kama vile yalitolewa zawadi, Kamati imeshindwa kuona kwamba kwa nini madeni haya hayalipwi. Kama trekta ni rasilimali linafanya kazi, linalima na wengine wanakodisha ina maana watu wote waliokopa matrekta wanatakiwa wayalipe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulizungumza, mwaka mzima sasa umepita hapa, hatuoni juhudi zozote. Kwa hiyo tulishawishi bunge liazimie kwamba hawa Suma JKT na wenyewe ambao hawasimamii ukusanyaji wa madeni waweze kuchukuliwa hatua na pesa za Serikali zisipotee. Hilo ni jambo muhimu sana kwa sababu uzoefu unaonesha kwamba mali ya umma inapotea hivi hivi kienyeji, lakini hiyo ni pesa ya Serikali na ni pesa ambayo inatakiwa irudi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pia iliweza kupitia, utendaji kazi katika mashirika mbalimbali na Wizara mbalimbali. Ukiangalia ukurasa wa 25 wa kitabu cha wasilisho la PAC kipengele 2.2.6 ambacho kinazungumza ununuzi wa magari ya polisi yenye thamani ya dola za Marekani milioni
29. Jambo hili lina lenyewe lina utata mkubwa sana na utata wake ni kwamba pamoja na nia njema ya jeshi la polisi, lakini mkataba huo hauna maelezo yakinifu kuonesha kwamba uliingiwaje, ulifanyikaje na huo mkataba utamalizika lini, yaani hayo magari mengine, yatakuja lini. Kwa sababu ukisoma pale utaona idadi ya magari yaliyoletwa ni kidogo kulingana na yaliyohitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mkataba huo wa Exim Bank ya India ambao uliingia ulifikia mahali ukawa ume- expire, hiyo credit facility ikawa ikawa ime-expire kabla ya utekelezaji wake kukamilika. Kwa hiyo sisi tunahoji tija ya mkataba huo na namna ulivyoingia na tunashauri kwamba lazima lifanyike jambo kubwa au maamuzi mazito kuhakikisha kwamba mkataba huo unakamilika na pesa za Serikali kuna mahali zilitolewa dola milioni 10 kama advance zijulikane ziko wapi. Kwa maana hiyo sisi tunaishauri Bunge tuweke azimio kuwe na reviw due deligency ya jambo hilo lote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ukienda ukurasa 21, suala la TANESCO, TANESCO inawadai watu wengi madeni. Mashirika mengi yanadaiwa, tulizungumza tena hili jambo lishazungumzwa na linarudi tena kuzungumzwa na TANESCO hawa, wanaonekana wanahangaika sana lakini pesa ziko kwa wateja, sasa tunashindwa kuelewa kwamba tatizo ni nini na kwa nini hatua hazichukuliwi. Kamati ilipata mashaka sana, nami napata mashaka sana, kwa sababu mashirika mengi ofisi nyingi zinahamia Dodoma Makao Makuu na madeni yako Dar es Salaam, sasa wanahamia Makao Makuu huku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaona ule msukumo wa kulipa madeni utakuwa ni mdogo, pamoja na kwamba, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alisema kama ni umeme kata sasa watakatiwa Dar es Salaam wanakuja kuanzia maisha huku upya, sasa jambo hilo na lenyewe inabidi liangaliwe ili liweze kuwa kuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba, jana tumepitisha hapa Sheria ya kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, lakini ukiangalia ukurasa wa 20 utaona madeni ambayo Serikali inadaiwa na mifuko ya jamii. Jambo hilo ni muhimu kwa afya ya Mifuko. Kwa hiyo, bado tunalishawishi Bunge liazimie kuona kwamba Serikali inalipa hayo madeni kikamilifu. Ukiona hilo jedwali linaonesha Mifuko na madeni na kiasi kinachodaiwa. Kwa hiyo, tunashawishi jambo hilo lifanyike kwa nguvu zote na Bunge liazimie kuona kwamba madeni haya yanalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Mifuko hii wanasema ifanyiwe actuarial valuation, inakwisha sijui mwaka gani, yaani maisha yake bado inaonesha yana uhai, lakini Kamati inapata mashaka kama pesa hizi bado ziko Serikalini, sasa hata hiyo actuarial valuation inakuwa pia ina mashaka kidogo. Kwa hiyo, tunalishauri Bunge lione umuhimu lione umuhimu wa kuhakikisha kwamba madeni yanalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda ukurasa wa 37 umiliki wa taasisi ya ukuzaji maendeleo Pride Tanzania Limited, hapa Kamati kwa kauli moja inasema tu Pride Tanzania, irudi Serikalini kwa sababu ndiyo iliyotoa mtaji mkubwa, lakini baadaye ikahamishwa inaendeleshwa na utaratibu na watu wengine. Kwa hiyo, tunasema pride irudi kwa sababu mtaji ulitoka Serikalini. Kwa hiyo, tunaomba Bunge na Wabunge wenzetu tutakapofika kwenye maazimio, tuone umuhimu wa pride kurudi Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho katika kuchangia leo nataka nizungumze kidogo kuhusu bandari, na TRA uhusiano wake wa kutokurejeshwa kwa mapato ya wharfage. Jambo hilo ni muhimu sana kwa sababu bandari zetu zinaendelezwa kwa hizo pesa, ambazo pesa hizo kimsingi zinakusanywa na TRA, lakini tunatambua kwamba TRA ni wakala tu na pesa zinakwenda moja Benki Kuu, Hazina wanatakiwa warudishe hizo pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tungependa labda Waziri mhusika atakapojibu hoja aseme kwamba kwa nini pesa hizi hazirudishwi, kwa sababu tunatambua kwamba kuna pesa nyingi hazijarudishwa ambazo zingetumika kwa maendeleo ya bandari zetu.

Mhemishiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na naomba Bunge likisoma maazimio tuyapokee maazimio yote kwa pamoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kuweza kunipatia nafasi ya kuchangia hotuba hii muhimu jioni ya leo. Kwanza kabisa niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa juhudi inazochukua ili kuweza kukuza uchumi, tumeona kwamba uchumi unakua kwa asilimia 6.8 na Tanzania ni moja miongoni mwa nchi tano za Afrika ambazo uchumi wake unakua vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye taarifa tumeelezwa zaidi ya viwanda 3,000 vimeweza kuanzishwa. Kwa hiyo hiyo ni hatua nzuri na ni dhamira ambayo Serikali ilivyoingia madarakani ilionesha kwamba jambo hilo litaweza kufanyika. Juzi tumeshuhudia pia uzinduzi wa lot two ya ujenzi wa standard gauge, hiyo ni hatua kubwa ya kuweza kuimarisha uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia Waziri Mkuu akizunguka maeneo mbalimbali kuhimiza suala la kilimo, kilimo cha pamba kinakwenda vizuri, korosho zimepanda bei na mazao mengine ambayo yameainishwa hapa mazao ya kimkakati. Sasa pamoja na pongezi hizo yapo mambo machache ambayo Wabunge inabidi tushauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianzia na kilimo, ule wigo wa mazao ya kimkakati uko umuhimu wigo huo ukapanuliwa. Kwa mfano, juzi Rais alizindua kiwanda cha mafuta cha alizeti Singida. Sasa zao la alizeti na lenyewe linatakiwa lipewe mkakati Dodoma, Singida na Shinyanga tuweze kulima zao la alizeti na tukilima zao la alizeti kwa wingi tunaweza kusaidia kuokoa fedha za kigeni ambazo zinatumika kuagiza mafuta nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, humu Bungeni huwa tunalumbana sana suala la kusema mafuta nje yasiagizwe, lakini mbegu zilizopo ndani ya nchi zinakuwa hazitoshi, sasa ni lazima uwekwe mkakati ikiwepo, kuwepo na ruzuku ya mbegu na mbolea ili zao hilo liweze kuzalishwa kwa wingi na tuweze kuvuna mazao ambayo yataleta tija kwenye viwanda vyetu, kwa sababu viwanda hivi vinategemea sana sekta ya kilimo. Kwa hiyo, sekta ya kilimo ikiimarishwa tutaweza kupiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nimeambiwa kwamba kuna malighafi ngano inaagizwa nje ya nchi na baadhi ya Wawekezaji ndani ya nchi humu, lakini zamani NAFCO walikuwa wanalima sana ngano na ilikuwa ni ya . Kwa hiyo, ni lazima mazao kama ngano na yenyewe yaweze kuangaliwa na tuweze kuyawekea mkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kuzungumza ni suala la elimu, nitazungumza kidogo sana kwa sababu kila siku tumekuwa tunazungumza na Wabunge wamekuwa wakizungumza suala la ubora wa elimu. Nimejaribu kufanya utafiti tu hasa katika Wilaya mpya hizi. Katika Wilaya mpya unakuta kwanza miundombinu yenyewe haitoshi, unakuta Wakaguzi na Waratibu Kata wapo, lakini Waratibu na Wakaguzi hawana usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya kama ya Mkalama haina gari la Wakaguzi, sasa huo ubora wa elimu wameachiwa Mkuu wa Shule na Walimu, kama utaratibu ulikuwa umeweka kuwepo na Wakaguzi wa Wilaya na Waratibu wa Kata ilikuwa ni muhimu kuhakikisha kwamba na mambo yanayohusiana na kusimamia ubora wa elimu yanawekwa vizuri ilikuwa ni jambo la muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la Walimu hawatoshi katika ngazi ya shule za msingi na sekondari na pia tukizingatia kwamba suala la elimu bila malipo limeongeza udahili wa wanafunzi. Pia tunaomba suala la VETA liimarishwe, kuna tozo iliwekwa hapa, tumetembelea VETA hivi karibuni tukaona kwamba pesa zile hazirudi, kwa hiyo tunaishauri Serikali iweze kurudisha ile tozo iliyokuwa inatozwa kwa maana ya kupelekwa VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA ni chombo kizuri kimeanzishwa, kinafanya kazi vizuri tuna imani nacho, lakini wenzangu wamezungumzia suala la uwakilishi wa TARURA kwamba wapi tunakutana na TARURA ili tuweze kutoa mawazo yetu. Ni jambo la muhimu inabidi kuangaliwa. Pia bajeti ya asilimia 30 kwa 70 TANROAD na TARURA bado inaleta mashaka ufanisi wa TARURA, TARURA itakuwepo pale lakini haitakuwa na ufanisi sana kwa sababu pesa zinazopelekwa kule zitakuwa hazitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, tunaomba Serikali iweze kuangalia namna ya kuipatia pesa zaidi TARURA ili kubadilisha mfumo wa mgawanyo labda iwe 40 kwa 60. Tunafahamu kwamba barabara za lami ni gharama na barabara ikishakuwa ya lami inatakiwa iendelee kuwa ya lami lakini bado tunahitaji barabara za vijijini ili ziweze kutoa mazao vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya niipongeze Serikali kwa kutoa pesa kuimarisha vituo vya afya Tanzania nzima ikiwemo Mkalama tulipata milioni 300 za kununua vifaa na kasi ya ujenzi inaendelea vizuri na sasa wananchi watapata tiba na Serikali itaonekana kwamba ipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya msingi ambayo bado ipo hapa ni suala la Wilaya mpya ikiwepo Wilaya ya Mkalama. Sasa Wilaya mpya hazina hospitali za Wilaya, kwa hiyo kwa maelezo ama jibu ambalo lilitolewa na Naibu Waziri wa Afya asubuhi natumaini na Mkalama nayo mwaka huu itapata hospitali ya Wilaya. Bado tunasisitiza kwamba Wilaya mpya zote ziweze kupata hospitali, hilo ni jambo muhimu na ule mnyororo wa tiba uweze kukaa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme tunaipongeza Serikali kwa kuweka mikakati ya kuongeza umeme katika gridi ya Taifa, kuanzisha Stieglers Gorge na miradi mingine kama Kinyerezi I, II na III. Ni jambo zuri kuleta umeme ambao utasaidia viwanda na viwanda bila umeme haviwezi kuwa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiunganisha na hapo, suala la REA, REA inafanya kazi nzuri lakini bado katika baadhi ya Mikoa speed yake ni ndogo na scope yake kwa maana ya kwamba nguzo ngapi zinakaa katika kijiji ni jambo muhimu ambalo inabidi liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri muhusika kwa sababu alifika katika Mkoa wetu wa Singida na bahati nzuri alifika Mkalama na alifanya kazi nzuri na kuna mahali umeme umewaka lakini bado tunataka kwenye miradi ya REA II ambayo ilikuwa haijakamilishwa iweze kukamilishwa, maana yake nguzo zipo kule na waya zipo wananchi wanaangalia, sasa wanaanza kusema umeme tutauona lini, wanaanza kukata tamaa, lakini kwa juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano nafikiri jambo hili litakaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala moja la msingi, suala la maji vijijini. Hotuba ya Waziri Mkuu imezungumzia suala la maji vijijini, lakini katika bajeti tuliona kwamba kulikuwa na mradi wa vijiji 10, visima hivyo virefu vimechimbwa vipo lakini havijajengwa na ukiangalia bajeti nyingi kwenye Wilaya wanatoa milioni 400 mpaka milioni 600. Mradi mmoja kujenga ni milioni 400, ina maana kama umechimba visima 10 itachukua miaka 10 kuweza kujenga miradi hiyo ya maji. Kwa hiyo, hilo ni jambo ambalo inabidi litafakariwe upya na liweze kupatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba tuanzishe Wakala wa Maji, tumeanzisha Mfuko wa Maji lakini sasa ianzishwe Wakala wa Maji kama vile REA inavyofanya kazi.

Wakala wa Maji akianzishwa atakuwa na kazi ya kutafuta pesa na kutekeleza miradi na kukabidhi miradi. Jambo hilo litakuwa mwarobaini wa upatikanaji wa maji hasa vijijini. Kwa hiyo, jambo hilo na lenyewe tunashauri Serikali iweze kulichukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kupongeza baadhi ya taasisi, nipongeze TEA kwa sababu wanasaidia sana katika sekta ya elimu, wamefanya kazi kubwa sana na hata Jimboni kwangu wameweza kufanya kazi kubwa sana. Pia nipongeze TAMISEMI kwa kusaidia miundombinu na kuleta watumishi inagwaje bado tunahitaji watumishi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, naishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa sababu inatekeleza sasa ili kuunganisha Mkoa kwa Mkoa. Daraja la Sibiti linaendelea vizuri na kabla ya kuja huku nilifika Sibiti na wananchi wana matumaini sana na daraja la Sibiti, tukimaliza Daraja la Sibiti sasa tunatarajia kwamba barabara hiyo itajengwa barabara ya lami na kuweza kurahisisha usafiri wa mizigo na raia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Nishati
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninashukuru kwa kuweza kupata nafasi ya kuchangia Wizara hii jioni ya leo. Kabla sijaendelea niseme kwamba naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili namshukuru Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wengine wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya na sote tunaiona kazi hiyo. Jambo moja ambalo Waziri inabidi alifahamu ni kwamba kuna hadithi ya uyoga wa porini, ukienda porini ukikuta uyoga haujaguswa hata na ndege ujue huo uyoga ni sumu, kama uyoga umeparuliwa paruliwa ujue basi huo uyoga unaliwa. Sasa mishale anayopata maana yake kwamba anafanya kazi kubwa na watu wanaona kazi hiyo. Wengine tumeshakwenda naye mguu kwa mguu mpaka Majimboni kwetu kwa hiyo tunatambua ufanyaji kazi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa ambayo naiona kwenye Wizara hii, yawezekana wewe speed ya Waziri ni kubwa kuliko hao anaofanya nao kazi. Kwa sababu Waziri akitoa maagizo TANESCO wenyewe wanapumzika wanasubiri tena Waziri aende, sasa tunataka mfumo ufanye kazi. Kwa hiyo, ni jambo la muhimu sana Wizara isimamie mfumo kufanya kazi. Ndiyo maana watu wanasema TANESCO inabidi iangaliwe upya, pia TANESCO inatakiwe liwe Shirika vibrant na liwe customer focused. TANESCO ikifanya kazi kwa mfumo huo tutapiga hatua kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa iliyopo katika Jimbo la Mkalama na Mkoa wa Singida kwa ujumla ni kwamba REA II na REA III ilikuwa haijaanza. Kwenye ukurasa wa 55 tumeambiwa kwamba mkandarasi anaanza, sasa tunaomba mkandarasi afike na afanye kazi kwa ukamilifu. Jambo hili ni muhimu sana kwa sababu kuna maeneo umeme umewaka na maeneo mengine umeme haujawaka na wananchi wanasubiri umeme. Kauli mbiu yetu kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tunasema umeme utawaka vijiji vyote, hata mimi nikienda nawaambia umeme utawaka vijiji vyote. Sasa kama ndiyo kauli mbiu yetu basi umeme unatakiwa uwake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba nguzo zinapelekwa kidogo sana. Pale Ibaga umeme umewaka lakini maeneo mengi hayajapata umeme, kwa hiyo pale manung’uniko mengine yamezaliwa ingawaje kazi kubwa ya kuwasha umeme imefanyika. Ukienda Iyambi, Gumanga, Nkalakala, Kinyangiri, Iguguno umeme umewaka lakini vitongoji vyake au maeneo ya karibu kabisa hayana umeme. Scope hiyo inabidi iangaliwe ili watu wengi waweze kupata umeme lakini pia umeme ni biashara TANESCO waweze kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kwamba Serikali inatoa pesa nyingi kujenga vituo vya afya. Wizara ya Afya na TAMISEMI wametoa shilingi milioni 400 kujenga vituo vya afya lakini havina umeme. Nafikiri sasa ni wakati muafaka Waziri atakapo-wind up atoe tu agizo kwamba vituo vyote vya afya vilivyojengwa umeme upelekwe, kwa sababu upasuaji na vipimo vitafanyikaje? Jambo hilo naona limesahaulika halafu tunaanza kupeleka maombi TANESCO inakuwa ni changamoto. Kama majengo yanakabidhiwa kwamba yamekamilika basi na umeme unatakiwa uwe umefika. Jambo hili pia tutazungumza na Waziri wa Maji ili na maji pia yaweze kufika kwenye vituo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali kwa juhudi zake za kuja na energy mix, kwa kuleta vyanzo vya umeme kwenye Grid ya Taifa kwa mifumo mbalimbali.

Umeme ulipokuwa unakatika tulikuwa tunalalamika kila siku sasa umekatika na siku hizi tuna mitandao wanasema sasa umeme umekatika, lakini katika kutekeleza azma hiyo huu mradi wa Stiggler’s Gorge nafikiri umeleta matatizo kidogo kwa baadhi ya watu. Umeleta matatizo kwa sababu tu ya kuwa na fikra mgando kwa sababu ni lazima utumie rasilimali uliyonayo ili uweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya rasilimali tuliyonayo ni hilo bonde na umeme wake unahitajika na kama study zimeshafanyika tangu mwaka 1950 na 1960 hakuna jambo jipya ambalo tunafanya sasa hivi. Kwa hiyo, jambo jema ni kushauri mradi huo utekelezwe vipi na hapa tunawashauri wataalam wetu wa mazingira waweze kusimamia kikamilifu jambo hili na mradi utekelezwe lakini tuupokee mradi badala ya kuanza kuuzuia kwamba usiweze kutekelezeka. After all Serikali imeshaamua kutekeleza nani anatakayezuia tena, kwa hiyo, mradi unaenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda mpaka Tanga. Bomba hilo litapita katika Mkoa wa Singida na katika Wilaya ya Mkalama ambako mimi ndiye Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki. Tunaiomba Serikali iangalie na isimamie kwa ukamilifu suala la fidia, pia suala la watu watakaofanya kazi katika bomba hilo katika Wilaya hizo au Mikoa husika waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema hivi kwa sababu mara nyingi maandiko huwa yanakuwa mazuri sana, tunapokutana kwenye presentation, tunapotaka kuanza mradi mambo yanayozungumzwa yanakuwa roses, yote yanakuwa ni maua mazuri lakini mradi unapoanza ndipo changamoto zinakuja. Kwa hiyo, tujifunze kutokana na makosa, hatutarajii kwamba mradi huu utaleta malumbano na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunategemea kutakuwa na quarters za wafanyakazi, kwa maana kwamba Wilaya hii au Mkoa huu utaleta wafanyakazi kadhaa na wafanyakazi hao waandaliwe, ikiwepo hata Mama Ntilie maana yake watapeleka vyakula katika maeneo hayo. Kwa hiyo, jambo hilo tukiliratibu vizuri nafikiri tutapiga hatua kubwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ni hili bomba la gesi wanasema linatumika kwa asilimia sita tu. Naona watu wengi tunasimama tunalaumu tu, lakini hayo ndiyo maendeleo na bomba lingekuwa limetumika asilimia 100 ingekuwa lime-fail. Sasa hivi tumeona gesi ya majumbani imeanza kutumika na viwanda vinatumia gesi. Kwa hiyo, tunatumai kwamba hili bomba sasa litatumika kikamilifu kulingana na capacity level. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni la msingi zaidi ni kwamba Mawaziri tunawahimiza kutembelea maeneo ya vijijini. Mkitembelea maeneo ya vijijini...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Waziri wa Wizara hii na Manaibu wake kwa kazi nzuri wanayofanya. Natoa shukrani zangu kwa kazi zifuatazo:-

(1) Kutoa fedha za jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Mkalamo;

(2) Kutoa fedha za uboreshaji wa Kituo cha Afya Kinyambuli (Tshs. 400m);

(3) Ujenzi wa Shule za Msingi (Kitumbili, Senene (TBA), Kibololo (TBA), Isanzu Secondary, Iguguno High School); na

(4) Kuleta wafanyakazi wa kada ya Walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunashukuru kutengwa kwa Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya. Pamoja na pongezi hizi naishauri Serikali kuona namna ya kutanzua changamoto zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, afya; naomba idadi ya watumishi waongezwe. Naomba Wizara isimamie kwa karibu shilingi bilioni 1.5 za Hospitali ya Wilaya, Wizara imekuwa mbali na miradi hii ambayo inagharimu pesa nyingi Serikali. Pia tunaomba ambulance.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu; miundombinu ya baadhi ya shule ni hafifu na haitoshelezi, naomba zipatikane pesa kusaidia wilaya mpya ya Mkalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukaguzi; tunaomba gari la ukaguzi, kwani ufaulu wa shule za msingi umeshuka kutokana na kutokuwepo ukaguzi (both) Waratibu wa Kata pamoja na Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara (TARURA); baadhi ya maeneo ambayo ni muhimu kwa uchumi wa wilaya na Taifa hayafikiki. Tunaomba fedha za barabara Msingi – Yulansoni – Lyelembo, kilometa 25.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na tunawaombea mfanye kazi yenu nzuri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nichukue fursa hii kumpongeza Waziri na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri wanayofanya. Nimechangia kwa kuongea, hata hivyo ipo hoja nyingine muhimu ambayo sikuizungumza kwa sababu ya muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, azma ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Jemedari Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli ni kuona sekta ya madini inatoa mchango stahiki katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, azma hii ni nzuri lakini takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa Serikali haina wathamini (Government Valuer) wa madini wa kutosha na hali hii imesababisha wawekezaji na wachimbaji wa madini kutoa takwimu za thamani ya madini kadri wanavyoona inafaa. Nashauri Serikali isomeshe wathamini wa kutosha na naomba wakati wa kuhitimisha hoja Bunge lielezwe hatua zilizochukuliwa katika suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.
Azimio la Kufuta Hasara itokanayo na Maduhuli ya Madeni ya Nyuma ya Ada na Leseni za Magari, Riba na Adhabu kwa kipindi kinachoishia tarehe 30 Juni, 2019
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii iliyopo mbele yetu. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PAC na hoja hii ililetwa na Waziri tukaijadili na leo tumeleta wasilisho letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifuatilia tutakumbuka kwamba, katika Hotuba ya Bajeti ya Mwaka 2017/2018, Bunge ndio pendekezo hili lilikuja na tukalipitisha kwamba, hiyo ada ya mwaka ifutwe, madeni, malimbikizo yote yafutwe na tulipiga makofi sana hapa. Ni kweli, ilionekana kwamba, ada hiyo inaleta kero, tulikubaliana, lakini kiutaratibu sasa wenzetu wale wa TRA hawawezi kufuta bila Bunge kuridhia na vitabu vyao vimeendelea kuwa na hesabu hiyo. Kwa hiyo, leo ni hitimisho tu la uamuzi ambao tuliupitisha wakati huo. Jambo lingine kubwa ni kwamba TRA watasafisha mahesabu yao na kumbukumbu zitakuwa sahihi, kwa hiyo utengenezaji wa mahesabu utakwenda na utakuwa umekaa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimeshangaa kidogo kusikia Kambi ya Upinzani kuleta hoja kwamba mjadala haukufanyika, Kamati ni Bunge dogo, kwa hiyo kule kwenye Kamati tulikojadili sisi tulijadili kwa niaba yenu. Mjumbe pia anaruhusiwa kuhudhuria kwa nini hakuja kule siku ile? Halafu jambo la pili amesema kiwango kinaleta mashaka CAG tunafanya kazi kufuata takwimu tunazoletewa na CAG na CAG alileta kuthibitisha jambo hili. (Makofi)

Sasa kama jambo limethibishwa na CAG labda aende yeye kukagua sasa ajipe Mamlaka mwenyewe aende kukagua. Kwa hiyo suala la kumbukumbu kuwa zina mashaka au kutokuwa na mashaka halina mantiki hapa, suala ni kwamba CAG amehakiki deni hili la Sh.398,845,888,750 na madeni yako mengi lakini hili ndiyo linahusiana na kufutwa kwa ada ya mwaka ya magari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naunga mkono hoja iliyoletwa na Waziri lakini na maelezo ya Kamati tunaunga mkono na jambo hili tusilifanye refu kwa sababu Bunge ndiyo lenye mamlaka, tufute tuendelee na kazi zingine. Tunaleta malumbano mengine ambayo hayana tija hapa, vinginevyo sasa tunaanza kufanya kazi ambazo siyo zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Madini
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nishukuru kwa kuweza kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu. Pia nishukuru kwa kupata fursa hii adimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nawashukuru Viongozi wa Wizara tukianzia na Waziri, Naibu Mawaziri wake wawili na timu nzima ya Wizara kwa kazi kubwa wanayofanya ya kufikia maeneo yetu ya madini. Sote tumeona jinsi kazi inavyofanyika, jinsi wanavyowajibika, tutakuwa wanyimi wa fadhila kama hatutawashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi yupo Mbunge mwezangu wakati anachangia alisemea suala la Tumuli, wachimbaji wa dhahabu walikuwa na mgogoro pale kuhusu mambo ya fidia lakini Naibu Waziri alifika Mheshimiwa Stanslaus Nyongo akaongea nao na aliongea kwa ujasiri mkubwa sana na alikuwa focused na aliweka msimamo wa Serikali na ndivyo nilivyotarajia. Kwa hiyo, alipoondoka pale nilikuwa niko vizuri sana kwa sababu hawa wawekezaji tusipokwenda nao vizuri wakati mwingine wanadharau vyombo vya Serikali, maadam tunasimamia haki kwa hiyo Waziri alifanya kazi kubwa sana na nampongeza kwa hilo pia natambua kwamba alikuwa anafanya kazi kwa niaba ya Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuna eneo la Dominiki wamegundua madini ya gypsum yanachimbwa huko lakini kulikuwa na mgogoro. Nachotaka kusema hapa ni kwamba Maafisa Madini walioko kwenye Kanda na Mkoa wakitoa leseni wao wenyewe waweze kufika katika maeneo husika ili kutoa taarifa hizo kwamba tumetoa leseni kwa mtu huyu na utaratibu ufanyike wa kulipa fidia na yule mwekezaji au mchimbaji aweze kufanya kazi yake bila migogoro yoyote lakini mwekezaji anapoibuka kunakuwa na mgogoro mkubwa usio na lazima na unaosumbua watu wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, eneo la Dominiki ni eneo ambalo linazalisha sana vitunguu, mwekezaji alivyofika akaanza kubomoa mashamba ya vitunguu, watu wakawa wanalinganisha gypsum na vitunguu maana vitunguu ndiyo maisha yao ya kila siku, kwa hiyo ni jambo ambalo ilitakiwa liangaliwe kwa undani ili tuweze kuona kwamba suala hilo litafanyika vipi kwa uzuri wake. Jambo hilo lilikuwa linaendelea na sasa hivi mambo yanakwenda yanatulia lakini tunachosema ni kwamba hawa Maafisa Madini wasilete migogoro isiyokuwa na sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala zima la reserve ya madini iliyopo nchini. Tunatambua kwamba kuna madini nchini na tunatambua kwamba kuna GST ni muhimu GST ikapewa pesa za kufanyia utafiti kujua reserve iliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema hivi kwa sababu tumeona katika baadhi ya maeneo tunategemea takwimu za wawekezaji kujua available resource iliyoko hapo, sisi hatuwezi kufanya projection, mgodi huu utafanya kazi kwa muda gani na tunatarajia kupata kiasi gani. Tunapopata hizo takwimu lazima ziwe proved na GST, kwa hiyo GST akipewa pesa za kufanya utafiti itakuwa ni jambo jema. Pia apewe na vifaa vya kisasa vya kufanyia ili waweze kwenda na teknolojia. Kwa kufanya hivyo, nchi itanufaika na ile sera ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ya kutaka rasilimali zetu ziweze kulindwa na Sheria mpya ya Madini itakuwa na manufaa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri utafiti wa maeneo gani yenye madini ufanyike Tanzania nzima na hasa katika maeneo ambako Serikali ina ubia kupitia STAMICO. Hilo ni jambo muhimu sana ambalo inabidi tuliangalie, yapo maeneo kama Mwadui, TANGOLD, Buzwagi, maeneo kama hayo yakifanyiwa utafiti tukajua rasilimali iliyopo hapo itakuwa ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo hilo tunao Maafisa Madini ambao wanafanya kazi kwa niaba ya Serikali. Ni wakati muafaka sasa kupitia Wizara lakini Tume ya Madini chini ya Prof. Mruma na mwenzake tuweze kuangalia suala la integrity, watu wanaopelekwa kule integrity yao iko vipi. Kwa sababu ukipeleka mtu ambaye anaweza ku- compromise ina maana rasilimali zetu zitakuwa zinapotea pasipo sababu yoyote. Tunatambua kwamba madini thamani yake ni kubwa, mtu aki-compromise pale anaweza kuwa anapata kitu kidogo lakini kwake yeye ni kikubwa kulingana na thamani lakini anakuwa analiumiza Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni ajira za wazalendo. Ni lazima tuangalie mgawanyo wa ajira kama zimekaa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Board Members. Je, Board Members walioko huko wana uwezo wa kutafsiri, wanajua wanachokifanya au tunawapeleka tu bila kuangalia uwezo wao? Kwa sababu kuna maeneo mengine professionalism inawapiga kando, unakuta wanakwenda kwenye bodi wakikaa wanakunywa chai wakitoka hapo wanapitisha wanakwenda. Kwa hiyo, suala zima la usimamizi linatakiwa liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuhusu STAMICO, kwa heshima kabisa na taadhima STAMICO wamekuwa wanatuangusha sana. Ni wakati muafaka Mheshimiwa Waziri na Wizara waangalie kwamba kuna nini huko STAMICO ili waweze kufanya kazi ambayo ilikusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuchangia ni suala zima la wachimbaji wadogowadogo, mikopo ya vifaa imekuwa ikitolewa, lakini bado manung’uniko yapo. Ukiona kuna manung’uniko maana yake utaratibu hauko wazi au hauko vizuri, unaweza ukakuta misaada hiyo inakwenda kwenye baadhi ya maeneo tu. Kwa hiyo, ni vizuri ikafanyika sensa wachimbaji wadogowadogo wakajulikana na mahitaji yao yakajulikana na kinachopatikana kikawekwa kwenye mgawanyo mzuri sasa kwamba tunapeleka huku na huku na huku. Hili ni jambo la fairness pia ni la ku-promote hao wachimbaji wadogo wadogo kwa sababu baadaye nao wanakuwa wakubwa pia wana mchango mkubwa katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maafisa Madini tunaomba wapatikane kwa urahisi katika maeneo yetu. Ziko Wizara zingine ambao Maafisa wao wanapatikana kwa urahisi lakini bado Maafisa Madini hawapatikani kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa, yuko mchangiaji amezungumza suala la magari makubwa kuja kuchukua madini. Kwa mfano, gypsum Dominiki malori yamekuwa yanakuja semi trailers yanabeba hayo madini, lakini tunapata ushuru mdogo sana kama Halmashauri madaraja yamevunjika na barabara zimeharibika anayezikarabati ni nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo muhimu sana tukaangalie ile compensation ambapo wananchi wa maeneo hayo waliothirika wanaweza wakapata kukawa na balance, kwamba madini yakachimbwa lakini barabara na madaraja yakatunzwa. Kwa sababu hatuwezi kushabikia uchimbaji wa madini wakati kuna uharibifu mwingine ambao unatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na hayo ya kusema, naunga mkono hoja lakini nampongeza Waziri na Naibu Mawaziri, tunaomba muendelee kuchapa kazi. Watu wanasema mbele kwa mbele hakuna kurudi nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kuweza kupata nafasi ya tatu ili kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa na Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti wa Mwaka 2019/2020. Kwanza kabisa niipongeze Wizara na wataalam kwa kazi kubwa wanayoifanya na kwa kutuletea hizi nyaraka. Nyaraka hizi zimekuja zioko vizuri tu, zisingekuja hizi nafikiri watu wasingekuwa na maneno mengi ya kusema, lakini nyaraka hizi zimeandikwa kwa umahiri mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipenda nianze kwanza kuhusu mwenendo na viashiria vya uchumi. Napenda niseme jambo kidogo hapo, ndugu zangu nafikiri wapo Waheshimiwa Wabunge huwa hawarejei tulipotoka, lakini Mheshimiwa Waziri katika Bunge lililopita alikwishaweka vigezo, unaposema uchumi unakua na projection ni 7.2 maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimshauri tena Waziri hilo darasa atakapokuwa anahitimisha aweze kulifungua tena kwa sababu wapo watu wana ubishani ambao hauna takwimu. Hata hivyo, pia wanachanganya sana kukua kwa uchumi na suala la umaskini, upimaji wa umaskini una vigezo vyake na kukua kwa uchumi kuna vigezo vyake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ukurasa wa nane kwenye hotuba ya Waziri napenda nizungumzie suala la uhimilivu wa deni la Taifa. Jambo hilo pia katika kikao kilichopita lilishafunguliwa darasa humu tunapimaje uhimilivu wa deni la Taifa. Niipongeze Serikali kwa kuwa wazi kwa sababu Serikali imesema deni la Taifa limekua kutoka dola za Marekani milioni 25 mpaka 27, kwa hiyo, Serikali haina jambo la kuficha hapa imeeleza wazi na vigezo vya upimaji viko wazi. Kwa hiyo, hao wanaotaka kubishana na takwimu inabidi wajipange ili waweze kueleza hili jambo kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze tena Wizara, Wizara imetuletea documents tatu, nafikiri wengine hawana au hawajazisoma. Moja ya document inasema taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kipindi cha mwaka 2016/2017 mpaka 2018/2019, ukifuatilia hapo utaona mambo makubwa ambayo yameshafanyika ndani ya miaka mitatu. Sasa watu wanaposema mpango unafeli sasa inakuwa ni changamoto kubwa sana. Nawashauri waende wakasome tena na hiyo Waziri hana sababu ya kuwajibu kwa sababu wanazo hizo nyaraka za rejea ambazo wanaweza wakasoma wakiwa mahotelini kwao au kwenye nyumba walizopanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la makusanyo ya mapato. Napenda nijikite kwenye suala la ukusanyaji wa mapato yanayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania. Tumeona wamekusanya asilimia 89, kwanza niwapongeze asilimia 89 kwa watu ambao wanajua ukusanyaji wa mapato hiyo ni A na wamefanya kazi kubwa sana ukizingatia wapo watu wengine wanataka kukwepa mapato kwa hiyo kunakuwa na ushindani. Kwa hiyo, TRA wamefanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona changamoto za ukusanyaji wa mapato, lakini moja ya eneo ambalo lilizungumzwa na ambalo tumekuwa tukizungumza ni suala la sekta isiyo rasmi. Ni muhimu TRA wakaa chini wakaangalia namna ya ku-formalize hiyo sekta isiyo rasmi. Jambo kubwa ambalo limekuwa linaleta changamoto ni viwango vikubwa vya kodi au viwango visivyo rafiki. Kwa hiyo, hawa watu tunaotaka kuwa-formalize lazima tufanye utafiti tuone tunawaingizaje kwenye wigo wa kodi, kwa hiyo wanaweza wakaanza kidogo tukawatambua; tukiwatambua, tukawalea watakuwa wanakua kidogo kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili nalisema kwa dhati kabisa kwa sababu natoka vijijini; kumekuwa na malalamiko makubwa sana na mengi kuhusu viwango vya kodi na utaratibu mzima wa ukadiriaji. Kwa hiyo, niwashauri wenzetu wa Mamlaka ya Mapato wakae watoe mapendekezo ambayo mapendekezo hayo yataweza kuwashawishi watu kuweza kulipa kodi badala ya kukwepa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ugharamiaji wa miradi ya kielelezo. Kabla sijafika kwenye ugharamiaji wa miradi ya kielelezo niseme kwenye ukusanyaji wa Mamlaka ya Mapato lazima tuangalie zile nguzo kuu za uchumi, tukiimarisha nguzo kuu za uchumi, tukiimarisha nguzo kuu za uchumi tutegemee makusanyo mengi kutoka kwenye kodi za ndani. Hii biashara ya bidhaa kutoka nje kuingia huku ndani ikikata tunakuwa hatupati mapato ya kutosha. Kwa hiyo, lazima tuhakikishe kwamba uchumi wetu unaweza kuongeza ukusanyaji wa mapato katika ile idara ya kodi za ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugharamiaji wa miradi ya kielelezo. Ugharamiaji wa miradi ya kielelezo ni jambo muhimu sana, miradi imeanishwa na ilianishwa tangu tulivyowasilisha mpango wa miaka mitano na mara nyingine wenzetu hawa wanakuja kusema hiki kimetoka wapi, lakini wakichukua kile kitabu cha mwanzo kabisa wataweza kuona miradi hii yote imetoka sehemu gani. Kwa hiyo, ni muhimu fedha zikatolewa na fedha hizo zitolewe kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la mikopo na misaada kutoka nje. Takwimu zinaonesha kwamba hatukuweza kufanikiwa sana na sisi tulitegemea sana huko, sasa lazima tuweke mpango mkakati imara wa kuona kwamba hilo jambo haliwezi kuturudisha nyuma, tuhakikishe kwanza vyanzo vyetu vya mapato tunavifanyia utafiti wa kutoka na tunaangalia associated risk kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sekta ya kilimo; sekta ya kilimo na yenyewe ipo kwenye suala zima kuna miradi ya kielelezo kule kuna mashamba ya sukari na vitu vya namna hiyo. Nipendekeze kabisa kwamba mpango huu lazima uangalie namna ya kumsaidia mkulima wa kawaida (mkulima mdogo). Wakulima wadogo hawana access na mikopo, kwa hiyo wakulima wadogo wakiweza kupata mikopo wataweza kuchangia kwenye kilimo ambayo ni malighafi, malighafi hiyo itakwenda kwenye viwanda. Hilo ni jambo muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia kwenye vyombo vya habari juzi tu mbegu ya alizeti kilo moja Sh.35,000; sasa nani anayeweza kumudu Sh.35,000 na akalima na huo uzalishaji wake umepimwa wapi. Ni muhimu jambo hilo likaangaliwa na yale mazao ya kimkakati yakafuatiliwa kwa karibu kama ambavyo Waziri Mkuu amekuwa akifuatilia suala zima la zao la pamba na korosho. Sasa na zao la alizeti lifuatiliwe. Kama tuliongeza kodi kwa mafuta yanayotoka nje ni muhimu mazao kama alizeti yakapewa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo ukipita ukitoka Shelui ukaja Singida, Dodoma mpaka Gairo yapo mafuta mengi sana barabarani wananchi wanashika yapo mkononi. Je, kuna mkakati gani wa kuweza kuyaingiza hayo mafuta kwenye mzunguko wa kawaida (ulio rasmi) na wale wananchi wakaweza kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala zima katika sekta ya afya, tulizungumza mwanzo, suala la ugharamiaji wa maboma ambayo nguvu za wananchi zilitumika. Jambo hilo bado halijapata jawabu lake. Tumejikita kuweza kutoa fedha kujenga vitu vya afya na Hospitali za Wilaya tunashukuru, lakini yapo maboma mengi sana ambayo wananchi waliyajenga na walitarajia Serikali iwasaidie kufunika. Tunaomba jambo hili na lenyewe liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelezo hayo marefu, nishukuru Serikali kwenye mipango mikakati yake kwa kuweza kuboresha miundombinu kwa sababu miundombinu ni mhimili mkubwa wa uchumi ikiwemo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa mzungumzaji)

MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya Kamati yetu. Mimi natoka Kamati ya PAC, kwa hiyo, hiyo hotuba ni ya wana-PAC wote. Nilivyoona makofi mengi yanatoka upande wa Upinzani nikawa najiuliza maswali mengi sana lakini kumbe hoja hii ilitakiwa isijadiliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kuweka kwenye record ni kwamba watu wanaotaka ile verification report iletwe, maana ule haukuwa Ukaguzi Maalum ilikuwa ni verification, hili jambo nalo lifahamike. Mheshimiwa Halima Mdee alikuwepo, Mheshimiwa Ester Bulaya alikuwepo na Mheshimiwa Zitto Kabwe tulikuwa naye. Hata dakika ya mwisho Mheshimiwa Zitto Kabwe alivyokuwa anatoka alituachia maswali ya kuuliza kwa ziada kwa maana tulijua ni Mbunge mwenzetu na tuliuliza yale maswali kupata ufafanuzi kwa sababu kila mtu alitaka ajue ufafanuzi wa shilingi 1.5 trilioni imekwenda wapi.

Nataka kuonesha tu kwamba kama alivyosema mwenzangu kwamba wapotoshaji wako humu humu badala ya kuchukua taarifa wanakuja ili waweze kupotosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo tunaliomba Bunge liweze kuzingatia Maazimio manne yale ambayo hayajatekelezwa kwenye ripoti iliyopita yaweze kufanyiwa kazi. Vilevile, tunaomba Maazimio ya Kamati..

T A A R I F A

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Allan Kiula kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mwambe.

MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo taarifa siipokei. Namheshimu sana Mheshimiwa Mwambe, lakini nafikiri kwamba anatulisha matango mwitu hapa. Hapa subiri tutoe taarifa na ambazo nyingine tumezinukuu ziko humu, tumefanya quotation, maana yake Kamati haiwezi kuleta quotation za uongo, quotation zilizoko humu ni quotation sahihi na kama unafikiri unaweza kunitoa kwenye reli huwezi. Ni mti mkavu usiochimbwa dawa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiendelea na uchangiaji wetu kuhusu trilioni 1.5 CAG kwenye verification report yake ameonesha hesabu zake zime-balance, hesabu zake zimewiana mapato na matumizi. Tumeona kwamba, zilipatikana trilioni 26 ukiangalia kwenye ukurasa wa 24 na matumizi kulikuwa na over release ya shilingi bilioni 290 na over release aliyoieleza inasababu yake, BOT walitoa kibali cha over release ya 1.2 trillion Serikali ikatumia bilioni 290 tu. Kwa maana nyingine kungekuwa na jambo ambalo si sahihi wangeweza kutumia pesa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu, Serikali imeonesha transparency ya hali ya juu kuruhusu Mfuko Mkuu wa Serikali kuweza kukaguliwa na CAG na kueleza mambo yote yaliyoko mle ni jambo kubwa sana. Si hivyo tu, watu wote tunafahamu kwamba ukaguzi unapofanyika wanaangalia checks and balance na wanatoa hoja kwa hiyo, hoja ni kitu cha kawaida na baada ya ripoti hii kutolewa Machi ndipo ilipokwenda kufanyika verification report. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walikuwepo na ndio maana nasema wapotoshaji walikuwepo, maelezo yaliyotolewa na CAG…

MBUNGE FULANI: Wapeeee!

MHE. ALLAN J. KIULA:...na mtu anayehojiwa alisema kwamba wakati ripoti inatolewa ziko transaction ambazo zilikuwa hazijawa recorded. Moja ya transaction ni pesa ambazo zinakwenda direct to project, unapopeleka pesa direct to project wakati gani una-recognize? Na watu wengine, wafadhili wetu (development partner), wanapeleka vifaa na nini kwenye project moja kwa moja.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiula kuna Taarifa nyingine. Mheshimiwa Profesa Ndalichako.

T A A R I F A

MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hiyo na kwa taarifa za ziada ndio maana niliamua niende kipengele kwa kipengele. Kwa sababu watu wamesoma humu uhasibu, wamesoma kodi, sasa tunataka tuoneshane hapa tumekwenda hatua kwa hatua na twende sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndio maana tumezungumza suala la pesa ambazo zilikuwa zimekuwa over spent na pesa nyingine za Zanzibar zilikusanywa Zanzibar na zilibaki Zanzibar, kwa hiyo, ile verification report ilikwenda kufanya usuluhishi wa takwimu zote hizo kwa undani wake na CAG mwenyewe akakiri na kwenye Hansard inaonesha na kitabu hiki kinafanya nini, kinaonesha kwamba usuluhisho ulifanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yapo mambo yalijitokeza na mambo hayo yaliyojitokeza ambayo Kamati ilihoji na tukapata kinachoendelea kule Hazina, tunaipongeza Hazina kwa ku-adapt hii Integrated Financial Management System inafanyika. Lakini pili, pia kuna single treasury account. Hayo mambo yote yalitakiwa yafanyiwe kazi na yakifanyiwa kazi kwa wenzetu wanaojua kuangalia haya mambo utaona kwamba zile hesabu zitakwenda sawa, sasa na taarifa, system zitaongea pamoja na taarifa zitaweza kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, suala la kwamba kwa nini kulikuwa na hoja, data zimekwenda kuwa marched hizo data. Kwa hiyo, suala la 1.5 trillion ni suala ambalo limekuwa closed, limeshahitimishwa na CAG alisema suala hilo limehitimishwa, alisema suala hilo limekwisha hitimishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo iko hoja ya TIB Development, kuna madeni kule kama tulivyoeleza kwenye taarifa yetu. Tunaomba Serikali suala hilo ilifuatilie na ilifuatilie kwa sababu madeni hayo ukiangalia huku ndani takwimu kwenye ukurasa wa 61 na 62, naomba kunukuu kwa kusoma inasema; “Katika jedwali 24 hapo juu inavyofafanua ni dhahiri kuwa kundi la mikopo inayohesabika kama hasara (loss loans) inachukua karibu asilimia 69. Kwa hiyo, TIB pia ina- operate chini ya required capital. Hasa hilo ni jambo muhimu sana ambalo Bunge tuazimie kwa sababu kwenye maazimio yetu yapo na Serikali iweze kulifuatilia kwa karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tulilizungumza na tumelipitia tena ni suala la mikopo ya matrekta. Tunaamini kabisa kwamba haijafanyika juhudi kubwa ya kuweza kukusanya madeni hayo kwa sababu, tunaamini madeni hayo yanakusanyika na kama wenzetu wakichukua hatua za makusudi kuweza kufuatilia tunaweza ku-recover hizo pesa ambazo ni pesa za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na mchango wangu ndio huo na suala la 1.5 trilion ni chapter closed. Nashukuru sana, asanteni. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye hoja iliyo mbele yetu. Kwanza kabisa, niseme mwanzo kabisa naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuunga mkono hoja, napenda niseme maneno machache ya utangulizi. Cha kwanza tunatoa pongezi kubwa kwa Serikali ya Awamu ya Tano ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa inayofanya. Sote tumeshuhudia Waziri Mkuu ametembea karibu mikoa yote Tanzania akifanya kazi kubwa za kuleta maendeleo ikiwepo kuhamasisha shughuli za maendeleo na usimamizi mzuri wa fedha za umma na hiyo imeleta ari kubwa kwa wananchi kuona kwamba Serikali yao inafanya kazi nzuri na kazi iliyotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna msemo unaosema Roma haikujengwa kwa siku moja, sasa watani zetu kila wakisimama hapa wanasema jambo hili halijafanyika, tunakwenda polepole lakini katika miaka hii minne sote tumeshuhudia kazi kubwa ambayo imefanyika. Hivi tunavyozungumza Rais alikuwa Kanda zile za Kusini alikuwa anafanya kazi kubwa ya kuhamasisha maendeleo na kufungua miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, ziko kazi kubwa zimefanyika ambazo zimeshazungumzwa na kwenye kitabu zimeandikwa kwa hiyo sina sababu ya kuzirudia lakini Watanzania wote wanaona kazi hizo. Napenda kuzungumza jambo moja kwa msisitizo sana nalo ni kilimo kwa ujumla wake. Watanzania wengi zaidi ya asilimia 70 wanategemea kilimo, sasa tunapozungumza kwenda kwenye uchumi wa kati na chenyewe kinatakiwa kibadilike, tupate ukombozi wa kilimo. Ili tupate ukombozi wa kilimo tunaelewa uchumi wa Watanzania, tunao wakulima wadogo wadogo wanalima kwa jembe la mkono na sehemu zingine wanalima kwa kutumia ng’ombe, kwa hiyo, hawawezi kujikombo katika suala zima la kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba limezungumzwa suala la kuimarisha Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo. Napenda kushauri kwamba benki hiyo iimarishwe na tuione vijijini kwa sababu unakuta benki hizi zinanufaisha baadhi ya watu wa mijini ambao pia siyo wakulima. Kwa hiyo, benki hii ikifika vijijini tutaweza kuwasaidia wakulima wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala zima la mazao ya kimkakati. Tumeona Waziri Mkuu ameweka juhudi kubwa kuhimiza kilimo cha pamba, korosho lakini pia alikwenda Kigoma kushughulika na mambo ya michikichi. Sasa uko umuhimu tupige kampeni kubwa sana kuimarisha zao la alizeti kwenye mikoa hasa ya kati ambapo zao hili linastawi.

Mheshimiwa Spika, pia tuangalie namna ya kuwasaidia hawa wakulima na wafanyabiashara wadogo wadogo wanaokaa na mafuta barabarani. Waziri wa Viwanda aangalie namna anavyoweza kuwasaidia mafuta hayo yakakusanywa lakini yakawekwa kwenye mzunguko yakiwa na viwango. Jambo hili tumekuwa tukilizungumza sana kwenye Wizara ya Viwanda tunasema kwamba mafuta ya kula yanatumia fedha nyingi za kigeni, jambo hili likifanywa vizuri tunaweza tukaokoa fedha za kigeni lakini pia tukainua uchumi wa Watanzania na Taifa letu likawa limekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukijikomboa katika sekta ya kilimo, tutakuwa tumepunguza pia umaskini. Kwa hiyo, dhana ya umaskini na yenyewe itakuwa imepewa suluhisho la kudumu. Tumeona juhudi mbalimbali zimefanyika, kuna mradi ule wa matrekta pale Kibaha, ingeangaliwa namna ya kuweza kusaidia wakulima wetu wa vijijini na pia tuweze kuwapanga vizuri ili waweze kulima maeneo makubwa kidogo na walime kilimo chenye tija.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni sekta ya elimu. Tunaipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo imefanyika. Sisi tunaotoka majimbo ya vijijini hiyo kazi tunaiona. Kwa hiyo, mtu anayesimama hapa Bungeni akasema hajaona kazi hiyo wengine sisi tunamshangaa.

Mheshimiwa Spika, isipokuwa pamoja na kuendelea kutoa Elimu Bila Malipo yako mambo makubwa ambayo yamefanyika, kwa mfano, ujenzi wa maabara lakini baadhi yake bado hazina vifaa. Kwa hiyo, naomba vifaa vya maabara vipatikane, technicians na walimu kwa sababu tunasema elimu ndiyo ufunguo wa maisha. Kwa hiyo, sekta ya elimu tukiimarisha tutaweza kupiga hatua kubwa.

Mheshimiwa Spika, si hivyo tu bali iko mikoa na jamii ambazo ziko nyuma kielimu, kuna maeneo ambayo hata hayafikiki. Kwa hiyo, tunaomba Ofisi ya Waziri Mkuu ifanye tathmini na kuona maeneo hayo yanasaidiwaje na hizo jamii zinasaidiwa kwa kiwango kipi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano rahisi tu, kuna pesa ambazo Serikali inatoa kusaidia kwenye shule kuboresha miundombinu lakini utakuta zile sehemu ambazo ziko nyumba hazipewi kipaumbele, unakuta mtu anacho halafu anaongezewa. Nashauri utengenezwe mkakati wa makusudi ili kuwe na uwiano wa elimu na jamii zingine zisije zikaachwa nyuma.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hilo hilo, niipongeze Serikali kwa sababu Mkoa wa Singida tumepata kama shilingi
1.3 ambazo ziligawanywa katika kila Jimbo ili kufunika maboma. Hata hivyo, bado tunasisitiza kwamba Serikali iangalie namna ya kutenga pesa zaidi ili zile nguvu za wananchi zisiweze kupotea. Tumeona miradi kama hiyo ni mizuri sana, Mwenge umepata fursa ya kufungua miradi hiyo, viongozi wanakuja, Mawaziri, Waziri Mkuu, Rais, Makamu wa Rais wanapata nafasi ya kufungua miradi hiyo ambayo inasaidia kuboresha mazingira ya utoaji wa elimu.

Mheshimiwa Spika, kwenye sekta ya nishati, kazi kubwa imefanyika, tunapongeza upatikanaji wa vyanzo vya umeme, ujenzi wa Stigler’s Gorge, Kinyerezi, Rusumo na maeneo mengine, kazi kubwa sana imefanyika na umeme huu ndiyo pia utasaidia viwanda. Kuna huu utekelezaji wa Mpango wa REA III wa usambazaji wa umeme vijijini na yenyewe imekuwa ni changamoto kubwa, yako maeneo ikiwepo Mkoa wa Singida ambao utekelezaji wake unasuasua sana. Kwa hiyo, tunaomba Serikali kwa ujumla wake iweze kuangalia jambo hili, Waziri mhusika ameahidi kwamba atafika na tunaamini kwamba atafika ili umeme huo uweze kupatikana.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hilo napenda niseme tu comment moja kwamba mimi kwa mtizamo wangu wako watu ambao wamepewa madaraka hawaisaidii sana Serikali kwa maana ya kwamba Mawaziri wanapokuwa wanafanya ziara, Mawaziri wa sekta zote, yanafanyika maandalizi mazuri na wanapofika pale wanapata taarifa nzuri lakini sasa wakiondoka utekelezaji wake unakuwa ni changamoto. Kwa tunaomba jambo hilo liweze...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kiula.

MHE. ALLAN J. KIULA: Naam!

WABUNGE FULANI: Muda umeisha.

MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nishukuru kwa kuweza kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu. Awali kabisa niseme naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, niwapongeze viongozi; Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya. Pongezi hizi msingi wake mkubwa ni kwamba watu wengi tunasema hakuna amani lakini ukilala ukiamka salama maana yake amani ipo, hiyo ndiyo tafsiri yake kubwa. Sasa twende kwenye issues useme wapi umekwazwa au wapi hapaendi sawa, lakini ukitoa statement ya generalization haileti afya kwa Taifa hili wala haileti afya kwa Polisi wetu ambao wanatulinda mchana na usiku. Tukitoka hapa tunakwenda kuchoma nyama hapo Chako ni Chako baadaye tunakwenda kulala halafu unasema Polisi hawakulindi. Sasa sisi tutoke wenyewe tuanze kujilinda kama ni hivyo. Kwa hiyo, kazi ya Polisi ni ya kutukuka na tunawapongeza na tunaomba waendelee kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni pongezi kwa Polisi wote lakini pongezi kwa Polisi wa Usalama Barabarani. Taarifa yetu imetuonesha ajali na vifo vinapungua. Tumekuwa tukiwalaumu sana Polisi wetu wa Usalama Barabarani kwa kutubana sisi madereva maana yake sisi wenyewe Wabunge hapa wote ni madereva, sasa lazima tufike mahali tufuate sheria za barabarani, tusiendeshe sisi kama wafalme. Sheria tumetunga inauma kotokote, huwezi kuwatungia sheria watu ambao wako nje ya Bunge, sheria ikitungwa na sisi inatugusa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, nichangie hoja hii ya Waziri. Jambo la kwanza, amezungumza mzungumzaji aliyepita suala la kisera. Mimi niko Kamati ya PAC, katika hoja zetu nyingi ambazo tumekuwa tukizipitia tumekuwa tukimpa taabu sana Afisa Masuuli. Tulichogundua ni kwamba Afisa Masuuli ana kazi kubwa sana na ana risk kubwa sana kwa maamuzi yote na vitu vyote vinavyopita mezani kwake. Asimamie Fungu 14, Fungu 28, Fungu 29, Fungu 51, Fungu 93; inakuwa ni kazi kubwa sana. Tunashauri Wizara iangalie namna bora ya kupunguza risk hii kwa Afisa Masuuli mmoja anayesimamia mafungu matano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo nafikiri Wizara ya Fedha inahusika, wataliangalia waone ufanisi unapatikana vipi katika mazingira kama hayo. Hata changamoto za mikataba mbalimbali iliyoingiwa na ufuatiliaji wake, tumeona kwamba mwisho wa yote ufanisi unapungua kwa sababu Afisa Masuuli ana kazi kubwa, anatakiwa awe na jicho kama la mwewe, yaani awe anaona kila sehemu. Kwa hiyo, hilo ni jambo muhimu, liweze kuangaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala zima la NIDA. NIDA sasa hivi ndiyo habari ya mjini wanasema, kwa sababu Serikali imeamua kila Mtanzania apate kitambulisho. Kama kila Mtanzania inabidi apate kitambulisho basi Wizara inatakiwa isimamie jambo hili na tuhakikishie wote wamepata vitambulisho. Huko vijijini tumeona ofisi zimefunguliwa, Maafisa wa NIDA wamekwenda hawana vitendeakazi, wamepiga watu picha huko kwenye kata, watu wanauliza vitambulisho lakini vitambulisho havionekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuangalie tatizo limeanzia wapi, ni kwenye mkataba wa uzalishaji vitambulisho. Tunaomba Waziri atakapokuja hapa atuambie mwarobaini wa vitambulisho ni upi? Watanzania wote watakuwa wamepata lini vitambulisho, tupate commitment ya Wizara. Hilo ni jambo muhimu sana na sasa hivi tumeona transactions zote zinazofanyika ukifika kitu cha kwanza unaulizwa Kitambulisho cha Taifa, kwa hiyo, hii ni agenda kubwa na ni agenda ambayo inatakiwa iwe katika boardroom, viongozi wetu wa juu wasimamie jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni vituo vya Polisi. Nimeona kwenye hotuba ya Waziri amehamasisha wananchi kujitolea kujenga vituo. Pamoja na wananchi kujenga vituo na sisi tunawahamasisha huko kwenye mikutano yetu na kwenye kazi tunazofanya, isipokuwa bado upo ule Mkataba wa STAKA, hatujapata majibu yake ndani na nje ya Bunge, naomba tupate majibu. Maana kuna vituo vimejengwa vimeachwa, kama Mkalama kituo pale kinaanza kuoza sasa, kilikuwa cha ghorofa, kinaharibika, pesa nyingi zimeshawekwa. Manyoni kuna kituo, kilikuwa kijengwe kituo kingine Ikungi na maeneo mengine mbalimbali, Lushoto imetajwa kama mfano. Hilo ni jambo kubwa na vile vituo umefika wakati wake vimalizike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali au Wizara utuambie ni lini vituo hivyo vitakamilika na ituambie kwa uhakika kabisa na usahihi. Kwa sababu hiyo inakuwa ni pesa iliyotupwa. Hata kama ilikuwa ni pesa ya kimkataba lakini ni pesa ambayo inatakiwa iwe accounted for, tujue kwamba vituo hivyo vitamalizika lini, pamoja na kuhamasisha kwamba bajeti zaidi itengwe kwa ajili ya kujenga vituo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo jambo ambalo wananchi nalo wanataka wajue, yaani kuna wingu zito. Limezungumzwa ndani na nje ya Bunge na kwenye vyombo vya habari nalo ni suala zima la mikataba ya Lugumi, mkataba wa AFIS, tupate kauli ya Wizara, inasemaje, hilo jambo limeishia wapi? Kwa sababu zipo fununu pia kwenye Jeshi la Magereza ipo mikataba mingi inayomhusu Lugumi ambayo na yenyewe ni mikataba tata. Tunaomba Wizara itueleze hapa ili wote tuwe kwenye ukurasa mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa hapa suala la malipo yasiyo na nyaraka timilifu. Hata hoja nyingi za Mkaguzi Mkuu wa Serikali zinaibuliwa kwa sababu ya ukosefu wa nyaraka, unaanza kutafuta waraka mmojammoja. Limezungumzwa suala la sare hewa, sisi tunaamini katika mazingira ya kawaida Jeshi la Polisi siyo eneo la kujifichia, siyo kichaka pale. Kwa hiyo, tunaamini kwamba hizo sare zilinunuliwa na hili suala la nyaraka hewa, mafunzo hewa, sare hewa, Waziri utatuambia ufafanuzi tuweze kujua kinachoendelea ni kitu gani. Jeshi kwa ujumla wake lina nidhamu ya hali ya juu, tunatarajia kwamba nidhamu ianzie jeshini. Kwa hiyo, nidhamu ikiwa nzuri huko hata Wizara zingine na maeneo mengine watainga mfano huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala vitendea kazi tupongeze Wizara, wameleta magari na mimi Mkalama nimepata gari la polisi japo tunahitaji magari zaidi lakini tunashukuru kwa hicho tulichopata. Nimshukuru Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer Masauni alifika kule na aliongea na wananchi na walifurahia sana kwa hiyo, tunapongeza sana kwa kazi hiyo kubwa inayofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira, tumeona humu ndani askari wataajiriwa, tunaamini kwamba mnawapeleka mikoani, Mkoa ma-RPC wanawapangia vituo kulingana na uhitaji. Tumeona Wizara ya Elimu wamechukuwa hatua nzuri sana kujua mahitaji ya ualimu kwa kila shule kwa hiyo wanapanga huku walimu wanakwenda moja kwa moja kwenye shule husika. Sasa nafikiri na hata jeshi la polisi liige mfano huo na magereza wawe wanapanga wafanyakazi kutoka huku huku. Kwa sababu wakienda tunawaachia ma- RPC wanapanga siyo kwamba hatuwahamini wakati mwingine tunaona kuna baadhi ya wilaya au kuna baadhi ya maeneo yanahitaji polisi wengi zaidi alafu wanakuwa hawapatikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba za askari kuna pesa ambazo zimetolewa za kujenga nyumba za askari, tunaomba hizo pesa nazo mgao wake usimamiwe kutoka Makao Makuu. Tunatambua kwamba mmekasimu madaraka hayo kwa ma-RPC mikoani, lakini mjaribu kuangalia kwa sababu zipo wilaya ikiwepo Mkalama, hakuna hata nyumba moja ya askari. Sasa hizo pesa na zenyewe zinufaishe maeneo kama hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii naunga mkono hoja tena ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niseme maneno machache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, naunga mkono hoja. Pili, nitoe pongezi kwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima kwa jinsi wanavyofanya kazi, wanafanya kazi vizuri. Tunaelewa kwamba wameikuta Wizara ina changamoto mbalimbali lakini wanaendelea kupambana nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulikumbusha, tulipoingia Bungeni baada ya muda kidogo tuliwekewa fomu kwenye maboksi yetu pale tukaambiwa tuandike miradi yenye matatizo. Sasa kwangu iko miradi yenye matatizo na niliandika na haijachukuliwa hatua. Juzi alipokuja Mheshimiwa Makamu wa Rais, tulikuwa na Naibu Waziri, mradi wa Nyahau ulileta shida kidogo lakini Mbunge alikwishawasilisha. Mimi niliomba miradi yangu hiyo yote ifanyiwe audit na nilikuwa na maana yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka miradi ya Iguguno, Kikonda, Kidarafa na Mtamba ifanyiwe audit kwa sababu design na kilichojengwa siyo chenyewe. Tulikwenda na Waziri aliyeondoka mwananchi wa kawaida anasema tuliambiwa ma-tank mawili na visima vya kuchotea maji kadhaa. Kwa hiyo, mwananchi wa kawaida anazo data, mainjinia wetu kwa nini hizo data hawazifanyii kazi. Bado nasisitiza tunaomba miradi hiyo ifanyiwe audit lakini pia hiyo liability nimeshaihamishia Wizarani kwamba nimesema ziko changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, Waziri alipofika Kidarafa na Kikonda aliahidi solar. Mheshimiwa Waziri nilizungumza, nafikiri jambo hilo linafanyiwa kazi maana kuendesha miradi hiyo kwa kutumia diesel ni gharama kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kitabu nimesoma, ukurasa wa 167 kuna shilingi milioni 90 zimetengwa naomba ule mradi usome Lelembo. Kwa heshima kubwa Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Waziri naomba mradi huu usomeke Lelembo. Nikisema kwa heshima kubwa nina maana yangu na nina maana kubwa sana na ikibidi tuma wataalam wako wachunguze kwa nini nimesema hivyo na jambo hili nimezungumza na Mkurugenzi. Kwa hiyo, tumekubaliana pasomeke Lelembo, mradi ule uende ukakamilike na huu ni mradi mmojawapo yapo majenereta mapya kabisa pale yanaoza, naomba mkayachukue muondoke nayo, maana siyahitaji lakini najua watu wengine watahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie kuhusu malipo ya wakandarasi. Certificate za wakandarasi hazijalipwa miradi wa Nduguti, Kinyangiri na Ipuli, tunaomba waweze kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na mradi wa visima 10, kihistoria tuna vijiji 70 lakini vijiji ambavyo vina maji havifiki 10 isipokuwa ule mradi wa vijiji 10 ungefanya vijiji 20 viwe na maji. Tunaomba hiyo miradi basi itengewe fedha kidogo kidogo lakini pia tunaomba usimamizi, jicho la karibu muweze kuona utekelezaji wake unakwenda vipi. Hizi fedha mnazoweka huko na siasa za kwenye Halmashauri huko unakuta fedha zinakuwa diverted zinakwenda kufanya miradi mingine tena. Kwa hiyo, tuna miradi lakini inaanzishwa mingine, kwa hiyo, tunaomba jambo hilo liweze kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wa miradi. Wilaya nyingi mpya zina changamoto ya magari, tunaomba hata gari bovu sisi tutatengeneza. Yaani gari lile bovu kabisa lililoko Wizarani nyie mtupe, mimi niondoke nalo Bunge likiisha, halafu tutakwenda kulitengeneza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo lingine ambalo tulikuwa tukizungumza la vyanzo vya maji. Yako maji mengi wamezungumza Wabunge wengine ambayo yanatiririka. Kwenye Bonde lile la Msingi maji yanatiririka mpaka Nyahaa kule. Niliwahi kuuliza swali hapa la msingi kwamba utafiti unafanyika, hakuna namna ya kukinga yale maji? Kwa sababu sisi hatuna ile mito inayotiririka kwa mwaka mzima ili tuweze kupata maji, sasa hilo bonde likifanyiwa tathmini tunaweza tukapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwenye visima vilevile 10 tunaomba mtume auditor, visima vimechimbwa, watu wamelipwa wameondoka vingine havina maji na fedha ya Serikali imeshakwenda. Hilo ni jambo la muhimu sana la kuweza kuangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wamezungumzia suala la Force Account. Ni muhimu sana tukaangalia kama kuna uwezekano tukaenda kwa approach hiyo tunaweza tukaokoa fedha nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tulianzisha Mfuko wa Maji, wamezungumza Wabunge wengi, lazima tukubaliane kwamba unahitaji fedha na kama unahitaji fedha tunafanya nini. Sasa tukubaliane kama Bunge hapa, tuangalie chanzo mahali popote pale, fedha ya Mfuko ya Maji iende, kile kiwango tukiongeze ili tuwe na fedha nyingi kwenye Mfuko wa Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na fedha nyingi kwenye Mfuko wa Maji hizo fedha basi na zenyewe zionekane vijijini. Wamesema wenzangu hapa mijini wana miradi mingi ya wafadhili lakini vijijini watu wanahitaji maji. Kauli kubwa hapa watu wanayozungumza, kila mtu anazungumza suala la maji. Leo sijazungumzia asilimia ya upatikanaji wa maji vijijini kwa sababu wenzangu wameshazungumza. Tufikie mahali tuwe na takwimu sahihi ya upatikanaji wa maji vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii fupi. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia kwenye kamati hizi mbili ambazo leo ndiyo siku yetu ya kuwasilisha ripoti. Kwanza kabisa niwapongeze wenyeviti wa kamati hizi mbili kwa kazi kubwa waliofanya ya kutuongoza. Jambo la pili nimpongeze CAG kwa kazi kubwa aliyofanya kwa sababu kazi yetu imekuwa nyepesi kwani wao walifanya kazi kwa weledi wakatushirikisha na sisi tukatembea kwenye hoja ambazo waliziandaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo nipitie maeneo machache, eneo la kwanza ambalo nimeona ni muhimu kupitia ni suala la ukusanyaji wa mapato ambalo linafanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Hoja za TRA zimeelezwa katika kitabu ambacho mwenyekiti ameweza kukiwasilisha hapa kwenye ripoti hiyo. Kamati inachosisitiza ni kwamba TRA ni roho ya Serikali, ni roho ya nchi na bila mapato bajeti yetu tunayoipitisha inakuwa ni bajeti ambayo haiwezi kutekelezeka. Kwa hiyo, TRA ni chombo ambacho tunakitegemea sana kiweze kukusanya mapato na mapato hayo yagharamie bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ndivyo basi hayo mapungufu ambayo tumeyaona ya (outstanding taxes) kodi nyingi kutokukusanywa yanatakiwa kufanyiwa kazi. Hapa linahitajika suala la weledi, suala la uadilifu na suala la kufanya kazi kwa bidii. Kukusanya kodi ni kazi kubwa lakini wakiwa na watumishi wenye weledi kazi hiyo itafanyika na mara zote tumekuwa tukiona suala la mlundikano wa rufaa kwenye Mabaraza ya Rufaa. Kamati ndiyo tumesema kwamba Bunge liazimie kwamba hizo kesi zimalizike na fedha au kodi iliyofungwa huko iweze kukusanywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo kama ipo kodi ambayo inaonekana haiwezi kukusanyika na ili vitabu vya TRA viweze kukaa sawa, basi hizo kodi zifanyiwe utaratibu wa kuweza kufutwa. Kwa mfano juzi tulipata wasilisho la kusudio la kufuta kodi ambayo inatokana na ile ada ya magari ya kila mwaka. Kwa hiyo, TRA wanayo kazi kubwa ya kuweza kuhakikisha kwamba wanarekebisha mahesabu yao lakini na kodi wanaikusanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo ningependa kulizungumzia ambalo tumelizungumza kwenye kamati yetu ni suala la Wakala wa Majengo (TBA). Hilo jambo ni kubwa sana, katika kupitia mahesabu yao na katika kuzungumza na TBA yenyewe tumeona kwamba wana miradi mingi ambayo haijakamilika na hata katika utendaji wao tunaona miradi mingine sasa wanaanza kunyang’anywa zinapewa taasisi nyingine. Hilo ni jambo ambalo linaashiria alama nyekundu kwa maana ya kwamba iko changamoto inabidi itatuliwe hapa. Pamoja na hayo yote, tunachoshauri pia labda hao TBA sasa wasipewe kazi nyingine mpaka wamalize hizi kazi zilizopo. (Makofi)

Nafikiri hilo litakuwa ni jambo kubwa na ni jambo zuri na ni jambo ambalo linaleta heshima kwa TBA yenyewe, lakini kama wameshika miradi midogo midogo na miradi haimaliziki hiyo haiwezi kuwa na sura nzuri kwa Taifa lakini pia hatuwezi kufuatilia matumizi mazuri ya fedha za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Nyumba (National Housing Corporation) na yenyewe kuna miradi mingi ambayo haijakamilika na miradi hiyo imesimama. Tumetembelea baadhi ya miradi kama ilivyoelezwa kwenye ripoti na tunaona sasa kwamba pesa ya umma au shirika lenyewe linakwenda kupoteza pesa nyingi. Miradi hiyo iliyosimama bado wakandarasi wako kwenye site na wakandarasi hao kwenye site wanalipwa pesa bila kufanya kazi. Sasa hatima ya National Housing ni nini? Hilo ndilo swali la kujiuliza, kwa hiyo tunaomba Serikali iingilie kati iweze kuona namna bora ya kuhakikisha kwamba baadhi ya miradi inakamilika, sio miradi yote ichaguliwe miradi ya kipaumbele ambayo inaweza ikamaliziwa na hizo nyumba zikauzwa au zikapangishwa kutokana na mpango ambao wao wameweka. Sasa hilo ni jambo muhimu sana kwa sababu hizo nyumba zitageuka kuwa magofu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona Serikali imetoa pesa nyingi kukarabati vyuo vya ualimu, tunaipongeza Serikali kwa kutoa pesa lakini pesa hizo nazo zimekwenda kwa utaratibu wetu wa force account. Sasa tunaona liko tatizo kidogo la usimamizi, jambo hilo ni kubwa, wasimamizi wanatakiwa wasimamie ili pesa isiweze kupoteza. Nia ya Serikali ni nzuri, lakini pesa zikienda tija hiyo isipoonekana na yenyewe inakuwa ni changamoto kubwa kwa sababu pesa ya Serikali ambayo ni kodi haiwezi kupotea hivi hivi. Kwa hivyo tunasisitiza kwamba pale ambapo tunaona usimamizi haukufanyika vizuri ambao hawakusimamia vizuri wachukuliwe hatua kwa sababu pia inakatisha tamaa kuona kwamba pesa zinatolewa halafu kazi iliyokusudiwa haifanyiki kikamilifu. Tunawapongeza na Wizara wamejitahidi kufanya kadiri walipoweza isipokuwa kwenye eneo la usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari tumeiona na yenyewe wamejitahidi, kwa nyakati tofauti bandari sasa hivi inafanya kazi kubwa tunaona pesa nyingi zinaingia na walitoa gawio juzi tuliona lakini suala la mifumo inabidi liandaliwe, mifumo iliyopo iweze kukamlishwa ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na hayo machache ya kuchangia, naunga mkono hoja au wasilisho letu chini ya Mwenyekiti wetu mama Kaboyoka. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia kwenye kamati hizi mbili ambazo leo ndiyo siku yetu ya kuwasilisha ripoti. Kwanza kabisa niwapongeze wenyeviti wa kamati hizi mbili kwa kazi kubwa waliofanya ya kutuongoza. Jambo la pili nimpongeze CAG kwa kazi kubwa aliyofanya kwa sababu kazi yetu imekuwa nyepesi kwani wao walifanya kazi kwa weledi wakatushirikisha na sisi tukatembea kwenye hoja ambazo waliziandaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo nipitie maeneo machache, eneo la kwanza ambalo nimeona ni muhimu kupitia ni suala la ukusanyaji wa mapato ambalo linafanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Hoja za TRA zimeelezwa katika kitabu ambacho mwenyekiti ameweza kukiwasilisha hapa kwenye ripoti hiyo. Kamati inachosisitiza ni kwamba TRA ni roho ya Serikali, ni roho ya nchi na bila mapato bajeti yetu tunayoipitisha inakuwa ni bajeti ambayo haiwezi kutekelezeka. Kwa hiyo, TRA ni chombo ambacho tunakitegemea sana kiweze kukusanya mapato na mapato hayo yagharamie bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ndivyo basi hayo mapungufu ambayo tumeyaona ya (outstanding taxes) kodi nyingi kutokukusanywa yanatakiwa kufanyiwa kazi. Hapa linahitajika suala la weledi, suala la uadilifu na suala la kufanya kazi kwa bidii. Kukusanya kodi ni kazi kubwa lakini wakiwa na watumishi wenye weledi kazi hiyo itafanyika na mara zote tumekuwa tukiona suala la mlundikano wa rufaa kwenye Mabaraza ya Rufaa. Kamati ndiyo tumesema kwamba Bunge liazimie kwamba hizo kesi zimalizike na fedha au kodi iliyofungwa huko iweze kukusanywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo kama ipo kodi ambayo inaonekana haiwezi kukusanyika na ili vitabu vya TRA viweze kukaa sawa, basi hizo kodi zifanyiwe utaratibu wa kuweza kufutwa. Kwa mfano juzi tulipata wasilisho la kusudio la kufuta kodi ambayo inatokana na ile ada ya magari ya kila mwaka. Kwa hiyo, TRA wanayo kazi kubwa ya kuweza kuhakikisha kwamba wanarekebisha mahesabu yao lakini na kodi wanaikusanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo ningependa kulizungumzia ambalo tumelizungumza kwenye kamati yetu ni suala la Wakala wa Majengo (TBA). Hilo jambo ni kubwa sana, katika kupitia mahesabu yao na katika kuzungumza na TBA yenyewe tumeona kwamba wana miradi mingi ambayo haijakamilika na hata katika utendaji wao tunaona miradi mingine sasa wanaanza kunyang’anywa zinapewa taasisi nyingine. Hilo ni jambo ambalo linaashiria alama nyekundu kwa maana ya kwamba iko changamoto inabidi itatuliwe hapa. Pamoja na hayo yote, tunachoshauri pia labda hao TBA sasa wasipewe kazi nyingine mpaka wamalize hizi kazi zilizopo. (Makofi)

Nafikiri hilo litakuwa ni jambo kubwa na ni jambo zuri na ni jambo ambalo linaleta heshima kwa TBA yenyewe, lakini kama wameshika miradi midogo midogo na miradi haimaliziki hiyo haiwezi kuwa na sura nzuri kwa Taifa lakini pia hatuwezi kufuatilia matumizi mazuri ya fedha za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Nyumba (National Housing Corporation) na yenyewe kuna miradi mingi ambayo haijakamilika na miradi hiyo imesimama. Tumetembelea baadhi ya miradi kama ilivyoelezwa kwenye ripoti na tunaona sasa kwamba pesa ya umma au shirika lenyewe linakwenda kupoteza pesa nyingi. Miradi hiyo iliyosimama bado wakandarasi wako kwenye site na wakandarasi hao kwenye site wanalipwa pesa bila kufanya kazi. Sasa hatima ya National Housing ni nini? Hilo ndilo swali la kujiuliza, kwa hiyo tunaomba Serikali iingilie kati iweze kuona namna bora ya kuhakikisha kwamba baadhi ya miradi inakamilika, sio miradi yote ichaguliwe miradi ya kipaumbele ambayo inaweza ikamaliziwa na hizo nyumba zikauzwa au zikapangishwa kutokana na mpango ambao wao wameweka. Sasa hilo ni jambo muhimu sana kwa sababu hizo nyumba zitageuka kuwa magofu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona Serikali imetoa pesa nyingi kukarabati vyuo vya ualimu, tunaipongeza Serikali kwa kutoa pesa lakini pesa hizo nazo zimekwenda kwa utaratibu wetu wa force account. Sasa tunaona liko tatizo kidogo la usimamizi, jambo hilo ni kubwa, wasimamizi wanatakiwa wasimamie ili pesa isiweze kupoteza. Nia ya Serikali ni nzuri, lakini pesa zikienda tija hiyo isipoonekana na yenyewe inakuwa ni changamoto kubwa kwa sababu pesa ya Serikali ambayo ni kodi haiwezi kupotea hivi hivi. Kwa hivyo tunasisitiza kwamba pale ambapo tunaona usimamizi haukufanyika vizuri ambao hawakusimamia vizuri wachukuliwe hatua kwa sababu pia inakatisha tamaa kuona kwamba pesa zinatolewa halafu kazi iliyokusudiwa haifanyiki kikamilifu. Tunawapongeza na Wizara wamejitahidi kufanya kadiri walipoweza isipokuwa kwenye eneo la usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari tumeiona na yenyewe wamejitahidi, kwa nyakati tofauti bandari sasa hivi inafanya kazi kubwa tunaona pesa nyingi zinaingia na walitoa gawio juzi tuliona lakini suala la mifumo inabidi liandaliwe, mifumo iliyopo iweze kukamlishwa ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na hayo machache ya kuchangia, naunga mkono hoja au wasilisho letu chini ya Mwenyekiti wetu mama Kaboyoka. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuweza kunipa nafasi na mimi niseme maneno machache katika bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, cha kwanza naunga mkono hoja, cha pili natoa pongezi kwa Wizara kwa maana ya Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji na naposema watendaji namaanisha wataalam, hili suala la wataalam nasisitiza kwa sababu wakati mwingine tulikuwa tukichangia humu bila kuzingatia utaalam wa watu ndio maana tunakuwa tumekazana kukosoa. Lakini pia nipongeze Wizara kwa kufuta tozo 54 hii ni historia, watu wengi walitarajia labda vinywaji vitapanda bei na nini lakini sasa naona Mheshimiwa Dkt. Mpango amewapiga chenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ile tax ammnesty na kutolewa kwa extension nitoe pongezi na nisisitize tu kwamba Wizara iongeze juhudi za kufuatili hasa hiyo kodi iweze kupatikana. Lakini pia suala la biashara miezi sita, watu wanaoandikishwa TIN kupata ule msamaha kwa miezi sita ni jambo kubwa sana, isipokuwa katika kuchangia hapa nimesikia kuna kitu kinaitwa bajeti hewa. Sasa nilijaribu kujiuliza bajeti hewa ni kitu gani, lakini bajeti hiyo ikashushwa hadi trilioni 29.

Mheshimiwa Spika, kwa kumbukumbu waliosoma ile sura ya bajeti tuliona kwamba vipo vyanzo vimewekwa vyanzo hivyo ndio vinakwenda kwenye shilingi trilioni 33 na baadhi ya vyanzo hivyo ni kodi na mapato ambayo tutakutana nayo ambayo sio ya kikodi lakini kuna mikopo ya ndani na nje na kuna misaada, sana sana ninachoweza kusisitiza ni kwamba Wizara sasa ifanye close monitoring iweze kufuatilia hivi vyanzo hivi viweze ku- perform hilo ndio jambo kubwa, kwa sababu kila siku bajeti inakuwa kulingana na mahitaji na kuna commitment zinaongezeka kulingana na mahitaji, kwa hiyo hatuwezi kuwa tunarudi nyuma tunasonga mbele. Pia tutambue kwamba katikati huwa kuna mid review ambayo huwa inafanyika kuangalia hivi vyanzo vina perform vipi, kwa hiyo ni mambo ya kitaalam ndio maana nilisisitiza suala la wataalam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu mimi nikalizungumza kwa sababu nina uzoefu nalo kidogo ni suala zima la clearing and forwarding. Suala la kwanza ni kujiuliza kwa nini tulianzisha clearing and forwarding na wanatambuliwa na nani, ndio maana wengine waliochangia wakasema kuna WCO inawatambua, East African Custom Management Act ya mwaka 2004 inatambua jambo hilo, kwa hiyo jambo hilo ni kubwa sana, lakini pia tuangalie historia ya TRA zilikuwa taasisi tatu zikaunganishwa ndipo ikatoka TRA walikuwa wanafanya kazi vipi na kulikuwa na mapungufu yapi.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunakwenda ni suala la IT system, kwa hiyo hawa watu wa clearing wanatumia mtandao, kwa maana hiyo ni lazima tuangalia hawa watu tunaosema kila mtu a- clear mzigo wake tutamuwekea huo mtandao kwenye simu. Lakini kuna vibali kutoka kwenye taasisi mbalimbali hivyo vibali watavipata kwa utaratibu upi. Kwa hiyo jambo hili tusije tukaliendea kwa pupa lazima liwe na uratibu mzuri na liangaliwe kwa karibu na lengo kubwa Serikali iweze kupata mapato yake, kunaweza kuwekwa exceptional labda kwenye loose cargo au mtu amekuja na television yake moja airport jambo hilo linatakiwa liangaliwe lakini suala la kumbukumbu ni muhimu sana pamoja na kodi suala la kumbukumbu ni muhimu sana. Kwa hiyo jambo likiangaliwa kwa ujumla wake wamezungumza mambo ya ajira, lakini mimi nilikuwa naangalia modality ambayo tutakwenda kuitumia ni modality ipi kwa sababu hatutaki ku- frustrate suala zima la ukusanyaji wa mapato. Hilo ni jambo muhimu, tunaomba Mheshimiwa Waziri uweze kuliangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la kodi ya mafuta; ukurasa wa 60 wa kitabu wanasema kutoa ushuru wa forodha wa asilimia 25 kwenye mafuta ghafi. Mwaka jana tuliongeza kodi hapa, lakini mafuta yameendelea kuja na hakukuwa na upungufu wa mafuta/hakuna impact yoyote ya ile hatua iliyochukuliwa na Bunge ya mwaka jana na ziko sababu mbalimbali. mimi baadae nitaleta mapendekezo lakini nilikuwa nafikiri na ninaona hiyo itakuwa ni busara kwenye mafuta ambayo ni ghafi asilimia 25 au dola 250 kwa tani. Pia kwenye mafuta ambayo yako processed asilimia 35 au dola 300 whichever is higher maana yake kunakushuka wanapokuja ku-declare wanasema bei ya mafuta kwenye soko la dunia imeshuka.

Mheshimiwa Spika, mimi nilijaribu kuangalia takwimu mbalimbali nikaona zile bei kweli zinaonekana zinashuka. Kwa hiyo kama bei hizo zinaonekana zinashuka sisi tunapoteza kipato, kwa hiyo wakiweka ile tag ya dola 250 kwa tani au ukiweka tag ya dola 300 ina maana Serikali itapata mapato yake. Lakini pia tumezungumza hii sababu hili jambo ni muhimu sana kwa sababu huku tulisema ukurasa wa 62 nanukuu walisema; “ongezeko la ushuru wa forodha linatarajiwa kuhamasisha uchakataji wa mbegu za mafuta hapa nchini na kuongeza ajira viwandani na mashambani.” Sasa kama hilo ndio lengo na tunataka tuongeze uzalishaji wa mbegu hapa ndani na uchakataji lazima tuweke ile tag ili kuweza kuhamasisha huku lakini pia ziko measures Wizara ya Kilimo inabidi kuchukua ili kuhamasisha uzalishaji wa mbegu za ndani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo jambo hili nilipenda kulizungumzia liweze kunufaisha viwanda vya ndani lakini pia liweze kunufaisha wakulima kwa ujumla wake. Sasa hivi bei ya mashudu nikitoka hapo kuna mbei ya mashudu kwa mkulima ni shilingi 200 lakini bei hiyo imeshuka kutoka shilingi 400,300 mpaka imefika shilingi 200, kwa nini kwa sababu ya ada na tozo zingine ambazo hazikuzungumziwa kwenye tozo zilizofutwa. Kwa hiyo ningeomba kama ningeomba kabisa ile tozo ya shilingi 20,000 kwa tani iweze kufutwa itakuwa ni hatua kubwa sana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Allan malizia.

MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia naomba Wizara waangalie ili waongeze juhudi za formalization ya informal sector kwa sababu huko ndio tutakusanya kodi watu wawekwe kwenye mfumo wa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu. Nashukuru sana kwa sababu nakuwa mchangiaji wa kwanza na hili Bunge ni muhimu kwa sababu sasa tunamaliza miaka mitano.

Mheshimiwa Spika, cha pili, nampongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano; na Waziri Mkuu alipokuwa anatupitisha kwenye hotuba yake, alikuwa anatembea kwenye kazi ambazo zimefanyika. Ni kazi ambazo unaweza ukaziona kwa macho, ukazigusa na ukapapasa. Kwa hiyo, hayo siyo maneno matupu ila kazi zilizofanyika. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, napongeza Viongozi Wakuu wa Serikali akiwepo Makamu wa Rais. Vile vile siyo kwa umuhimu, lakini nikupongeze wewe Mheshimiwa Spika kwa kutuongoza kwa miaka mitano. Mambo mengi mazuri yamefanyika na mambo makubwa yamefanyika. Hili linalozungumzwa “Bunge Mtandao” watu waliona haliwezekani, lakini leo hii hata sisi tulikuwa tunafikiri Bunge baada ya Corona tutaendanalo vipi? Sasa jinsi ulivyolipima na kuliratibu Spika, basi umekuwa Spika mahiri sana. Nakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi, naanza kwa kuunga mkono hoja iliyowekwa mbele yetu. Yako mambo ambayo ningependa kuyazungumza kidogo, kutokana na mazingira tuliyonayo sasa hivi na angalizo langu liko kwenye suala la mapato; tuna sehemu ya matumizi na mapato. Leo hii wakati hotuba hii imesomwa, tuna changamoto ya ugonjwa huu, janga la Corona ambalo janga hili limefanya sekta nyingi zisimame au zisifanye kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pamoja na kwamba tunapitisha bajeti hii, nashauri sana Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara zinazofuata, pesa tutakazopelekewa wazitumie kwenye maeneo muhimu kwa sababu hatuna uhakika kama flow ya hizo pesa itaendelea hivi, kwa sababu mchango wa sekta mbalimbali za kiuchumi ikiwepo utalii, madini na sehemu nyingine tunaona kwamba zinaathirika na hili janga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya angalizo hilo nampongeza Mheshimiwa Rais kwa hatua alizochukua za suala nzima la kuangalia namna ya kudhibiti janga hili la Corona. Jambo la muhimu hapa ni usimamizi; tunasimamia vipi hizo hatua ambazo tumejiwekea sisi wenyewe? Hilo ni jambo muhimu sana, maana hii social distancing inatupa shida kidogo, lakini ni utamaduni ambao tunatakiwa tuuchukue.

Mheshimiwa Spika, tukifuatilia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, yako mambo mengi yamezungumzwa, kazi nyingi zimefanyika, zile nguzo kuu za uchumi ambayo ndiyo mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano zimeelezwa kikamilifu na hatua ambazo tumefikia. Sasa pamoja na mafanikio tuliyoyapata, tukienda kwenye suala la miundombinu; ujenzi wa reli ya mwendo kasi na maeneo mengine, kwa sababu Ofisi ya Waziri Mkuu inaratibu, basi zile rasilimali inatakiwa zisimamiwe kikamilifu ili miradi hiyo isiweze kuathirika na hali inavyoendelea sasa hivi. Nazungumza hali ya kiuchumi inavyoendelea.

Mheshimiwa Spika, Sekta mbalimbali zimegusiwa katika hotuba hii. Nikigusa Sekta ya Kilimo, Sekta ya Kilimo ni sekta muhimu sana. Kwa hiyo, tunamba Ofisi ya Waziri Mkuu ikaratibu Sekta ya Kilimo lakini imtambue mkulima mdogo, pia twende mpaka chini tumwangalie mkulima mdogo tuone tunamsaidia vipi? Kwa sababu tunapozungumza viwanda, malighafi zinatoka huko chini kwa wakulima wadogo wadogo ambao ni wengi. Kwa hiyo, ni jambo muhimu sana. Tunashauri jicho la karibu liweze kutupiwa huko.

Mheshimiwa Spika, tukienda kwenye Sekta ya Elimu, mambo makubwa yamefanyika na mafanikio makubwa yameweza kufanyika. Yapo mambo kadhaa ambayo inabidi yaangaliwe kwa karibu. Elimu bila ada imekwenda vizuri sana isipokuwa tumekuwa na changamoto ya miundombinu kwa maana ya madarasa, nyumba za walimu na walimu wenyewe. Kwa hiyo, ni eneo ambalo linatakiwa liangaliwe kwa karibu sana kwa maana ya uratibu. Wizara husika inafanya kazi vizuri, lakini eneo hilo linatakiwa liangaliwe vizuri likiwepo suala nzima la uratibu wa mikopo ya elimu ya juu. Hilo ni jambo muhimu pia.

Mheshimiwa Spika, Sekta ya Maji na yenyewe inahitaji kuangaliwa kwa karibu sana. Takwimu zimetolewa hapa zinaonyesha tunapiga hatua nzuri na tunaipongeza Serikali kwa hatua inazochukua na kwa uwekezaji mkubwa unaofanyika kwenye Sekta ya Maji, isipokuwa bado uko umuhimu wa kuhakikisha kwamba rasilimali kwenye Sekta ya Maji zinaongezeka hili tatizo hili liweze kutatuliwa. Tumeona kwamba maji vijijini sasa hivi ni asilimia 64, kwa hiyo, tunatarajia kwamba asilimia hiyo iweze kuongezeka kupitia huo Mfuko wa Maji.

Mheshimiwa Spika, miundombinu imezungumziwa. Atakuja Waziri mhusika kuzungumza habari ya miundombinu hapa, ninachokiona, mwaka huu tumepata mvua nyingi. Mvua hizo zimeharibu sana miundombinu kama barabara na madaraja. Kwa hiyo, chochote ambacho tutakuwa tumekipanga hapa kitakwenda kwenye miundombinu, lakini hakitakwenda kwenye kutengeneza miundombinu mipya, itakwenda kwenye kukarabati miundombinu hii. Kwa mfano, daraja la Kiyegeya halikuwepo kwenye mpango, lakini sas limeshatumia rasilimali kubwa. Kwa hiyo, suala hilo na lenyewe inabidi liangaliwe kwa ukaribu tuweze kuona tunasonga mbele vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema suala nzima la ukusanywaji wa mapato, sasa ni muda muafaka kabisa kupanua wigo lakini na Halmashauri zetu kuziwezesha. Siku za nyuma katika bajeti zilizopita, Halmashauri ziliombwa ziandike miradi ya mikakati; jambo hilo lilikwenda baadaye likasimama kidogo, lakini tunaiomba Ofisi ya Waziri Mkuu iweze kusimamia hilo jambo hili Halmashauri ziwe na hiyo miradi ya kimkakati ili ziweze kuzalisha mapato zaidi.

Mheshimiwa Spika, tukienda Sekta ya Afya, kazi kubwa imefanyika na takwimu kwenye hotuba ya Waziri Mkuu zimeonyeshwa dhahiri. Nami namshukuru Waziri Mkuu alifika hata Jimboni kwangu kule, alikagua hiyo Sekta ya Afya na alifanya kazi kubwa sana. Sasa hizo hospitali zilizojengwa zinahitaji vifaa na zinahitajika zianze kufanya kazi. Kwa nguvu kubwa iliyowekwa na ofisi zote kuanzia Mheshimiwa Rais, Ofisi ya Waziri Mkuu, sasa inatakiwa ionekane kule kwa wananchi kwamba hizo hospitali, zahanati na vituo vya afya, vinafanya kazi kwa kupelekewa vifaa.

Mheshimiwa Spika, fursa za uwekezaji zimezungumzwa kwenye hotuba ya Waziri Mkuu. Tumeweka nguvu sana na msukumo mkubwa kupata wawekezaji, mimi niseme wawekezaji wa nje. Sasa ni muhimu tukangalia namna ya kuwawezesha wawekezaji wa ndani, kuwawekea mazingira mazuri waweze kupata mikopo kwenye mabenki au kwenye taasisi nyingine za fedha lakini pia hata kuwasaidia kuona maeneo ambayo wanaweza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Allan.

MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma wa Mwaka 2017
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kuweza kunipatia nafasi ya kuweza kuchangia muswada huu muhimu. Pili, naipongeza Wizara na watendaji wote waliofanyia kazi Muswada huu kwa sababu umekuja kwa wakati muafaka kabisa. Kwa hiyo, wale wanaoona kama ungeahirishwa au haujatimia, mimi nasema muswada huu umetimia na ndiyo wakati wake kuwasilishwa na ninasema umechelewa sana kuletwa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, lakini yako mambo kadhaa ambayo inabidi tuyaangalie sisi kama Bunge na kuyatolea maamuzi. Mambo mengi yameshazungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu, lakini nami nitajazia baadhi ya sehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile section 19 inazungumzia suala zima la mwajiri kama atakuwa hajapeleka michango, yaani fursa ya mwajiri kutokupeleka michango. Uhalisia sasa hivi ni kwamba inapotokea hali kama hii uyo mfanyakazi ambaye amestaafu anastahili kulipwa mafao yake, huwa anapata shida kubwa. Kwa hiyo, hatutakiwi kutoa nafasi au fursa ya mwajiri kuchelewesha michango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sheria ingesema tu kama mwajiri anatakiwa apeleke michango kwa wakati inapo-fall due, basi, tukaishia hapo hapo. Kwa sababu nafahamu kwamba kwenye mifuko wako ma-inspector ambao ndio kazi yao kufuatilia michango hii. Kwa hiyo, siyo kazi ya mwanachama kufuatilia mchango. Kwa hiyo, hilo ni jambo la muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kipengele namba 22 kinasema: “money paid in excess.” Hili lilivyoingia tu kidogo lilinipa ukakasi, kwa sababu kama sasa hivi tuko kwenye mambo ya teknolojia (IT), kwa nini michango iende in excess halafu tuanze kuangalia inarudishwa kwa utaratibu upi? Kwa hiyo, hili jambo lingeweza kuangaliwa kwa sababu wao wanaopeleka michango wanatakiwa wawe makini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko jambo lingine kwenye kuunganisha mifuko ambalo na lenyewe lipo lakini sijaliona vizuri, labda Waziri mhusika atalifafanua. Wako wafanyakazi ambao walikuwa wafanyakazi, wameshachangia kwenye mifuko hii inayounganishwa, lakini sasa hivi sio wafanyakazi na hawachangii, lakini pesa zao bado zipo kwenye mifuko na hawajachukua. Walikuwa wanasubiri muda wa miaka 60 au 55 waweze kudai mafao yao. Sasa sijaona kwenye transition au hili jambo litakuwa handled vipi? Wako wengi sana wa namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ile section 29 inayozungumzia ile list ya mafao, Waheshimwia Wabunge wameshazungumza suala la health benefit, ni jambo muhimu sana likawekwa. Bunge hili lisikubali kupitisha sheria hii kama hilo jambo halitawekwa, kwa sababu jambo hilo ni muhimu na tumeona faida zake na wananchi wanahangaika. Mifuko mingine ilianzisha involuntary contribution, lakini kwenye involuntary contribution watu wanapata mafao na limeweza kusaidia sana Watanzania. Kwa hiyo, ni fao muhimu na ambalo ni muhimu likawekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuunganisha mifuko, huko nyuma tulizungumza kwamba litapunguza gharama za uendeshaji. Kwa maana hiyo tulitarajia kwamba gharama zilizopungua na wanachama wakiwa pooled kwenye mfuko mmoja, kutakuwa na ongezeko la kuondoa michango na kwa sababu michango hii itawekezwa ina maana kutakuwa na ongezeko la uwekezaji. Kwa hiyo, mafao kama health benefit na mengineyo, fao la elimu wamezungumza, ni muhimu yakawekwa kwa sababu ni jambo ambalo linawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine muswada huu umezungumzia suala la kwamba mafao hayatatozwa kodi. Sheria ya Kodi (Income Tax Act) section 10 (3) nafikiri inaeleza kwamba iwe ina-override mambo yote. Kwa hiyo, jambo hili labda Mheshimiwa Waziri aliweke vizuri ili atuhakikishie kwamba kodi haitatozwa kwenye mafao ya mwisho. Ni rahisi tu, ni kuongezea pale kwamba “not withstanding”, tunaongezea maneno pale, mambo yanakaa vizuri. Kwa sababu ni matarajio kwamba kwa kuunganisha mifuko, kutakuwa na manufaa zaidi na ndiyo imani ya Wabunge kwamba kutakuwa na manufaa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ndio ulikuwa huo na ningependa kusisitiza hayo mambo machache. Nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii.
Muswada wa Sheria ya Kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi wa Mwaka 2018
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia katika Muswada huu. Nami nilipigwa bumbuwazi kidogo, unajua Singida ni kilomita 240 tu mpaka kufika Dodoma sasa nikawa nafikiria kwenda kufuata huduma Dar es Salaam ambako nakwenda kilomita 720 sasa nikaona hilo ni jambo la kushangaza kidogo.

Mheshimiwa Spika, niseme uongozi ni kuonyesha njia na uongozi ni kuishi kwa maneno yako na kwa matendo hilo ni jambo muhimu sana. Sasa Serikali zote zilizopita suala la kuhamia Dodoma lilishapitishwa na uamuzi huo ulikwishapitishwa. Kwa hiyo, ilikuwa ni suala la kufanya maandalizi na muda muafaka ukifika ndipo jambo hilo litekelezwe. Sasa Awamu ya Tano ndiyo muda muafaka umefika, kwa hiyo, hilo nimpongeze Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kulivalia njuga suala hili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hivyo, hata wewe mwenyewe ulisema “Mkutano huu hautakuwepo, nikunukuu mwenyewe “Kama Muswada huu hautaletwa”. Kwa hiyo, nikupongeze na wewe pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ulisema kwa nia njema kwa maana ya Tanzania kwa ujumla wake. Ukiangalia sababu zilizotolewa kuhamia Dodoma jambo moja kubwa ilikuwa ni katikati ya Nchi, sasa sababu hiyo haijabadilika, ipo na itaendelea kuwepo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tulitaka huduma, wananchi wapate huduma karibu, tusogeze huduma kwa wananchi. Jambo hilo pia linaendelea kubaki na watu watapata huduma kama kawaida lakini lilikuwa ni so divested kwamba Dar es salaam ni Mji wa kibiashara na iko Miji mingi ya kibiashara Arusha, Mbeya, Mwanza ni Miji ya kibiashara sasa tuwe na Mji wa Serikali. Pia usalama wa nchi kwa hiyo, imeonekana Dodoma iko katikati na Serikali itakuwa salama ikikaa hapa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, yako mambo mengi ambayo yamekwishafanyika. Bunge hapa tuko tumeona Bunge tumekuwa na makao yetu makuu hapa, tunaendelea. Waziri Mkuu alishahamia, Ikulu ilikwishajengwa, Makamu wa Rais yupo, kwa hiyo, suala la white paper linakuwa ni suala ambalo halina tija na limepitwa na wakati kwa sababu uko uwekezaji ambao tayari umekwisha fanyika.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunasisitiza sisi ifanye white paper, lakini sisi Wabunge tuko mia tatu tisini na ngapi ndio tunaosema white paper lakini wananchi ndio shida yao hiyo white paper? Wananchi jambo hili wanasubiri utekelezaji wake tu kwa sababu lilishatolea uamuzi. Pia tumeona nchi nyingi zimechukua uamuzi wa kuwa na makao makuu ya Serikali wakahama kwenye miji ile ya zamani. Afrika ya Kusini tumeona, Abuja tumeona, China tumeona. Pia kwa kumbukumbu nzuri ni kwamba, hata Nigeria walikuja kujifunza hapa kabla ya kujenga Abuja, kwa hiyo, hilo lilikuwa ni wazo nzuri ambalo lilionekana kwamba, ni jambo muhimu kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa nikirejea kwenye uwasilisho MUswada, intent ya Muswada ni nini? Muswada huu, Muswada unapendekeza kutungwa, nanukuu “kutungwa kwa sheria na kulitangaza Jiji la Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi”. Sasa hilo ni jambo muhimu sana na sisi Wabunge tumekasimiwa nafasi hiyo na madaraka hayo. Kwa hiyo, ni muda muafaka wa kuweza kuunga mkono Muswada huu, tuupitishe na Dodoma iwe Sheria, sheria iwepo na Dodoma iwe Makao Makuu.

Waheshimiwa Wabunge kwa heshima na taadhima kubwa nasema jambo hili, nilifikiri mjalada utakuwa ni mwepesi sana kwa sababu ni jambo ambalo lipo na linaloendelea. Kwa hiyo, ilikuwa ni sisi kukamilisha tu, lakini inatokea kama sintofahamu, sasa sintofahamu isisababishe tukalitia Taifa hili hasara kwa sababu uamuzi ni kwamba Dodoma iwe ni Makao Makuu.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa tuliopo humu ndani tumeona Serikali imeweza kuhamia, sasa wakati mwingine uongozi lazima ufanye maamuzi magumu, ni magumu lakini yanatekelezeka. Kama huko nyuma tulilegalega, sasa yametolewa maamuzi magumu na uamuzi umetekelezeka, Wizara zote zimekwishahamia hapa, bado Rais tu ambaye na yeye tunamtarajia Mwenyezi Mungu akijalia mwaka huu na yeye aweze kuhamia Dodoma. Kwa hiyo, kumbe basi hata siku za nyuma tungekuwa tumechukua uamuzi mgumu huu tayari Dodoma ingekuwa imeshakuwa na sura nyingine kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali kuhamia Dodoma maana yake sio kwamba Jiji la Dar es Salaam, maana tunapozungumza kuhama Jiji la Dar es Salaam ndio Makao Makuu yalikuwepo, sio kwamba litadumaa linaendelea na shughuli zake ndio maana mnaona maendeleo ya Dar es Salaam yako pale pale. Bandari inapanuliwa, flyovers na barabara zinatengenezwa kama kawaida. Kwa hiyo, Tanzania yetu na yenyewe sasa inanufaika na Serikali kuhamia hapa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi ni jukumu letu sisi kuweza kutambua ukweli, ukweli ni nini? Ukweli ni kwamba uamuzi wa kuhamia Dodoma ulikwishafanyika, sasa sisi tukamilishe tu hilo jambo, lakini kwa manufaa yetu sisi Watanzania wa sasa hivi na wa vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja na naomba Wabunge wenzangu tuweze kuunga hoja hii, ili Dodoma iwe Makao Makuu kikamilifu kwa sheria. Naomba kuwasilisha.
Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalam ya Walimu Tanzania wa Mwaka 2018
MHE. ALLAN J. KIULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia Muswada huu ambao ni muhimu sana. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuweza kuleta Muswada huu, nasema umekuja kwa muda muafaka. Nasema hivi kwa sababu taaluma nyingi zimeona umuhimu wa kuweka udhibiti au kutambua watu ambao wako sahihi katika taaluma hiyo. Ndiyo maana kwenye wasilisho la Mheshimiwa Waziri amejaribu ku-cite baadhi ya taaluma ya Uhasibu, Ufamasia, Ukunga na kadhalika kuonyesha umuhimu wa kuwepo kwa Bodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri tu Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anajibu aweze kufafanua kidogo tofauti kati ya Bodi na Teacher’s Service Commission, kwa sababu hapa inaonekana upo mchanganyiko, huyu kachukua kazi za huyu na huyu kachukua kazi za mwingine. Kwa hiyo, hilo ni jambo muhimu sana. Ingawa Mwenyekiti wa Kamati alijaribu kufafanua lakini alikwenda kwa speed sana. Kwa hiyo, ni muhimu Waheshimiwa Wabunge tukafafanuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya maudhui ya kuanzishwa kwa Bodi hii ni kulindwa kwa hadhi ya taaluma na utalaamu wa ualimu kwa kuzuia watu wasiokidhi vigezo na viwango. Ndiyo maana kwenye maeneo mengine tumekuta kuna madaktari fake, waandishi wa habari fake; sasa nafikiri huu ndiyo mwarobaini wa taaluma ya ualimu kulindwa tukizingatia kwamba taaaluma ya ualimu ni taaluma yenye heshima kubwa na ni taaluma yenye mchango mkubwa katika Taifa hili na sisi wote tumetoka mikononi mwa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia kwenye Muswada, tukianza pale section 5, jambo la muhimu tunashauri kwamba uteuzi wa Kiongozi Mkuu au Mtendaji Mkuu ateuliwe na Rais, itakuwa ni jambo nzuri; Mheshimiwa Waziri ateue wajumbe wa Bodi lakini huyo Mtendaji Mkuu ateue watendaji kwenye maeneo ya wilaya ambako huko mbele imeelezwa ili kuwepo na mgawanyiko, kwa sababu yule mtendaji ndio anasimamia wale watendaji kwenye ngazi ya chini. Sasa hili ni jambo zuri ambalo inabidi liangaliwe na mwasilisha Muswada aweze kuangalia kama anaweza kuleta amendment ikawa imekaa vizuri. Nafikiri kazi hiyo ya Rais kuteua itakuwa haina uzito wowote ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, isipokuwa tukienda ukurasa wa saba, functions of the Board, kifungu cha 6(2) kuna kitu kimeandikwa: “In performing its functions under this Act, the Board shall collaborate with the Ministry with a view of ensuring that individuals who wish to be trained in the teaching profession, receive the requisite education and train for registration under this Act.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kwamba Wizara sasa inajivua hapa. Kwa nini Wizara isibaki na jukumu lake la kuhakikisha hilo jambo linakuwepo? Kwa hiyo, hii kazi haikutakiwa kupelekwa kwenye Bodi. Nashauri hapa pafanyiwe marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda section 9, delegation of power na penyewe nikapata mashaka kidogo, nikaona Bodi imeshaanza kuzidiwa kazi hata kabla haijaanza. Kwa hiyo, nafikiri suala la delegation kwenye kifungu kidogo cha (1) yote iwe deleted. Sababu pia aliposhuka chini kidogo kwenye kifungu kidogo cha (3) anasema, Notwithstanding subsection (1), the Board shall not have power to delegate its, zile powers zikawa zimelezwa pale. Kwa hiyo, suala la delegation nafikiri lote tu lingeachwa, Bodi iachiwe utaratibu wa kufanya kazi na majukumu yote Bodi iwe inawajibika kwa sababu tunapoanzisha kitu, tunataka hicho kitu kiwajibike. Tunasema tunaanzisha kitu kikubwa ili kiwajibike katika tansia hii ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda section 14(2)(a), kuna kitu pia nimeona kama hakijakaa sawa. Wanasema, conduct preliminary investigation on charges or complaints against teaching professionals on malpractise, lack of compentence, unajua ili tupate walimu bora huu mchujo unatakiwa uanzie kwenye admission, kwa hiyo, anapomaliza anakuwa amehitimu. Kwa hiyo, viko vitu ambavyo vitapimwa anapokwenda kufanya kazi, lakini suala la competence vyuo vyetu viwe vimefanya kazi ya kutosha kuona hao walimu wanaotolewa wanakuwa kweli ni walimu wameiva, ndipo twende kumpa leseni. Sasa mwalimu anatoka, mpaka unampa leseni anakwenda kupimwa kule na Bodi inaonekana kuna udhaifu huku kwenye chujio la kwanza. Kwa hiyo, chujio linatakiwa lifanyike kikamilifu. Sasa hilo na lenyewe lingeweza kuangaliwa kwa uzuri wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda ukurasa wa 10, suala la ku-reject an application, nilifikiri hii Bodi inaanzishwa inakuwa ni ya kisasa kabisa, kwa sababu kutakuwa na mambo ya IT na kila kitu. Kama IT ipo, ina maana ile application yenyewe itakuwa rejected unapotuma tu maombi yale, inakataliwa moja kwa moja. Kwa hiyo, hili jambo litakuwa halipo. Kwa hiyo, eneo hilo nashauri liondolewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la full time teaching na lenyewe napendekeza lifafanuliwe vizuri. Pia ukienda ukurasa wa 11, kifungu cha 21(2)(b)(iii), pale aliposema, the Board shall take into account any behavior of the applicant if, is unfit to be a teacher. Narudia kule ambako nilisema kwamba chujio la mwalimu linatakiwa lianzie mbali. Kwa hiyo, Bodi ilitakiwa ifanye mambo mengine, siyo hii kusema unfit to be a teacher. Hilo ni jambo ambalo linatakiwa liangaliwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni ukurasa wa 12, section 23 linazungumziwa suala la tozo. Hizo tozo kama Waheshimiwa Wabunge wengine walivyochangia, tunapendekeza kwamba tozo isiwe chanzo cha mapato na ziangaliwe zisiwe kikwazo. Nashauri registration iwe bure kabisa (zero) lakini kwenye annual fee ndiyo iwe inalipiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema registration iwe bure kwa sababu watu wanapomaliza chuo wanakuwa hawana pesa na hali zao ngumu. Kwa hiyo, kama hali zao ngumu, basi iwe zero ila huko kwenye annual fee ndiyo iwe inafanyika. Vinginevyo, tutashindwa kusajili watu wengi kwa sababu Serikali inaajiri walimu wachache na wengine wanaenda private sectors lakini wako watoto na kaka zetu mtaani na vyeti vyao wanazunguka. Sasa hivi tu hawana kazi, wakitakiwa walipe na hiyo registration fee itakuwa ni changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo niliona nilizungumzie kidogo ni suala la kusimamia nidhamu. Sasa imefikia wakati kama tunatengeneza mifumo au taasisi za kusimamia nidhamu. Huyu mwalimu anakwenda kusoma, maana kama degree anasoma miaka mitatu, kama diploma anasoma miaka miwili, sasa kule anakuwa hajawa vetted? Maana upekuzi unatakiwa uanzie kule, wenzetu wale kule kwenye vyuo waseme bwana wewe hufai, yaani kazi ya ualimu wewe haikufai. Kama mifumo ya huko itakuwa imekaa vizuri, hata nidhamu za walimu zitakuwa zimekaa vizuri. Kwa hiyo, Bodi itakuja kushughulika na mambo mengine tofauti na jambo la nidhamu. Vinginevyo, nidhamu huyu mwalimu awe amebadilika tu baada ya kuajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.