Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Elias John Kwandikwa (8 total)

MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
(a) Je, katika kipindi cha mwaka 2010 - 2015, ni ng‟ombe wangapi wametaifishwa na Serikali kwa kuingia katika Hifadhi ya Kigosi eneo linalopakana na Jimbo la Ushetu katika Kata za Ulowa, Ubagwe, Ulewe, Nyamkende na Idalia?
(b) Je, ni utaratibu gani unatumika kuua ng‟ombe wanaoingia kwenye hifadhi; na ni ng‟ombe wangapi waliuawa katika kipindi cha mwaka 2010 - 2015?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na utalii, kwa mara nyingine tena, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, chini ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Ibara ya 27(1), kila mtu ana wajibu wa kulinda maliasili ya Jamhuri ya Muungano. Aidha, Sheria ya Kuhifadhi na Kulinda Wanyamapori, Na. 5 ya mwaka 2009, vifungu vya 18(2) na 21(1) vinakataza mtu yeyote kuingiza mifugo, kuchunga au kulisha mifugo ndani ya Hifadhi za Taifa, Mapori ya Akiba na Mapori Tengefu. Chini ya kifungu cha 111(1) cha sheria hiyo, mtu aliyepatikana na hatia ya kuingiza mifugo ndani ya hifadhi atanyang‟anywa mifugo hiyo kwa amri ya Mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kubwa ya wafugaji kuingiza mifugo wengi katika Pori la Kigosi wanaohatarisha ustawi wa hifadhi hiyo. Serikali Wilaya ya Ushetu na Mkoa wa Shinyanga wamekuwa wakitoa elimu kwa wananchi juu ya athari ya kupeleka mifugo ndani ya hifadhi kwa Mapori ya Akiba na msimamo wa sheria.
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2010 - 2015 hakuna ng‟ombe waliotaifishwa na Serikali katika Wilaya ya Ushetu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imebaini kwamba watu wanaopeleka mifugo ndani ya mapori ya Kigosi/Moyowosi ni pamoja na wageni toka nchi ya jirani ambao wanaingia hifadhini na silaha za kivita. Katika jitihada za kuwatoa wafugaji wa aina hii katika hifadhi, maafa yametokea hapa na pale. Askari kadhaa Wanyamapori wamepoteza maisha, mifugo kadhaa wameuawa katika mazingira ya aina hii; hata hivyo Serikali haina sera, sheria, kanuni au utaratibu wa kuua mifugo.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Kata za Uyogo, Igwamanoni, Ushetu na Chena katika Jimbo la Ushetu hazina mawasiliano ya simu za mkononi ya uhakika. Je, ni lini maeneo hayo yatapatiwa mawasiliano ya simu za mkononi yenye uhakika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa naibu Spika, vijiji vya Manungu na Uyogo katika Kata ya Uyogo pamoja na vijiji vya Iramba, Luhaga, Mwamanyili kutoka katika Kata ya Igwamanoni na vijiji vya Mwazimba na Nundu kutoka katika Kata ya Chela vimekwishapata huduma ya mawasiliano kupitia utelekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi wa Kampuni ya simu ya Vietel.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vya Jomu na Buchambaga vya Kata ya Chela, vijiji vya Mhuge na Ibambala, Kata ya Ushetu na Kipangu na Igwamanoni Kata ya Igwamanoni vipo katika utekelezaji wa awamu ya pili na awamu ya tatu ya miradi ya kampuni ya simu ya Vietel ulioanza Novemba 2015 na kutarajiwa kukamilika Novemba 2017.
Aidha, kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote, vijiji vya Kata ya Ushetu, vijiji vya Bugoshi na Kalama kutoka katika Kata ya Uyogo na vijiji vya Chela, Mhandu kutoka katika Kata ya Chela, vitaingizwa katika awamu zijazo za mradi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Serikali imekuwa ikitumia waajiriwa wa muda (vibarua) ambao hawana ujuzi, uadilifu wala taaluma ya uhifadhi:-
(a) Je, ni vibarua wangapi walitumiwa katika Hifadhi ya Kigosi kwa kipindi cha miaka mitano (2010-2015)?
(b) Je, Serikali ilikuwa imetenga kiasi gani cha fedha na ni kiasi gani kililipwa kwa vibarua hao?
WAZIRI WA MALIASILI NAUTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya shughuli ambazo hazihitaji ujuzi mahsusi kama usafishaji wa ofisi, kufyeka barabara na mipaka ya hifadhi. Kazi hizo hutolewa kwa wananchi waishio kando ya hifadhi ikiwa ni njia mojawapo ya kuwapatia kipato na kukuza mahusiano mema kati Serikali na wananchi hivyo kuwapa faida za moja kwa moja za kiuchumi kutokana na kuwepo jirani na hifadhi. Aidha, wapo vibarua ambao hufanya kazi zinazohitaji elimu na ujuzi mahsusi wa wastani kama vile ukatibu muhtasi na udereva ambao huhitaji kuwa na vyeti na leseni zinazoruhusu kufanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida hakuna kibarua anayefanya kazi za kiuhifadhi moja kwa moja kwani kazi hizo zinahitaji taaluma, ujuzi na uzoefu wa masuala ya uhifadhi wa wanyamapori katika viwango vinavyokubalika na taaluma yenyewe. Ajira za vibarua hutolewa kulingana na mahitaji ya ofisi, hivyo wanaokidhi vigezo hupewa mikataba ya ajira kwa kipindi kisichozidi miezi mitatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Pori la Kigosi kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2010 - 2015 jumla ya vibarua 240 walifanya kazi za muda kama kufyeka barabara na mipaka na kusaidia kufanya usafi wa kambi na miradi ya maendeleo kama vile ujenzi wa nyumba, ukarabati wa majengo kwa kushirikiana na Askari wa Wanyamapori.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi hicho jumla ya shilingi milioni 27.8 zilitumika katika kuwalipa vibarua hao. Aidha, kampuni zinazoendesha shughuli za utalii katika mapori huajiri vibarua kwa ajili ya shughuli zao.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatambua mchango mzuri wa wasimamizi wa Rasilimali Fedha, Wahasibu Viongozi (Chief Accountants) walioko kwenye Wizara na Idara za Serikali kwa kuwapandisha kwenye ngazi ya Ukurungenzi ili waweze kuleta tija zaidi kwa ushirika wao katika maamuzi ya Menejimenti ya Wizara/Idara zao?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Jimbo la Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, cheo cha Mhasibu Mkuu au Chief Accountant ni cheo cha madaraka/uongozi na kwa mtumishi anayeteuliwa kushika wadhifa huu anakuwa na hadhi sawa na Mkuu wa Idara au Mkurugenzi katika Wizara au Idara ya Serikali inayojitegemea au wakala na Wahasibu Wakuu ni sehemu ya Menejimenti ya Wizara, Wakala, Idara za Serikali zinazojitegemea na wamekuwa wakishiriki kikamilifu katika maamuzi ya Wizara na Idara zao kama ambavyo wako Wakuu wengine wa Idara au Wakurugenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwapatia mafunzo ya awali watumishi na viongozi wa umma kabla ya uteuzi wa madaraka yoyote katika utumishi wa umma ili waweze kuuelewa utumishi wa umma na kufahamu misingi, sheria, kanuni na taratibu za utendaji kazi katika utumishi wa umma. Mafunzo ya aina hii yamekuwa yakitolewa na Taasisi ya Uongozi, Chuo cha Utumishi wa Umma pamoja na wakala wa mafunzo kwa njia ya mtandao au (TAGLA).
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na mauaji ya wazee na walemavu wa ngozi kutokana na sababu mbalimbali.
(a) Je, ni idadi ya watu wangapi waliopoteza maisha katika Jimbo la Ushetu kwa kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015?
(b) Je, mauaji ya makundi haya yanapungua au yanaongezeka katika Jimbo la Ushetu?
(c) Je, Serikali imeshirikisha vipi jamii kupiga vita mauaji haya, vikiwemo vikundi vya dini, walinzi wa jadi (sungusungu) na uongozi wa kimila Jimboni Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2010 wazee waliouawa walikuwa wawili, mwaka 2011 wazee wanne, mwaka 2013 wazee watano, mwaka 2014 wazee waliouawa walifikia sita, mwaka 2015 walikuwa wawili, mwaka 2016 wawili na mwaka 2017 alikuwa ni mzee moja. Kwa hiyo, jumla ya wazee ambao wamepoteza maisha katika kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwaka 2010 hadi 2017 ni wazee 22 katika Jimbo la Ushetu. Kwa upande wa walemavu wa ngozi, katika kipindi hicho hakuna mlemavu aliyeuawa wala kujeruhiwa Jimboni Ushetu ila kwa nchi nzima kwa kipindi cha miaka 2010 mpaka 2017 walemavu wa ngozi waliouawa walikuwa ni sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mauaji ya makundi haya katika miaka ya karibuni yanapungua kutokana na misako iliyofanywa ya kuwakamata waganga wa kienyeji ambao wanapiga ramli chonganishi na kuchochea imani za kishirikina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukomesha mauaji haya, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwemo kushirikiana na taasisi mbalimbali zisizo za Kiserikali ndani na nje ya Jimbo hilo katika kutoa elimu ya ukatili huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikishirikiana na jamii na taasisi za kidini, vikundi vya ulinzi jamii ndani na nje ya Jimbo la Ushetu kwa kuwapa elimu wananchi ili kudhibiti maujai hayo ya kikatili.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Polisi wamekuwa wakifanya msako na kamatakamata ya waganga wa kienyeji sehemu nyingi hapa nchini:-
(a) Je, ni waganga wangapi wa kienyeji walikamtwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu?
(b) Je, ni waganga wa kienyeji wangapi walifikishwa Mahakamani na kutiwa hatiani katika kipindi hicho katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, waganga wa kienyeji waliokamatwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu ni 26 na kushtakiwa kwa makosa ya kufanya biashara ya uganga bila kibali na kupatikana na nyara za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015 jumla ya waganga 16 walikamatwa na kufikishwa Mahakamani. Kati ya hao, waganga saba walipatikana na hatia kwa kufungwa miaka miwili kila mmoja au kulipa faini ambapo jumla ya watuhumiwa sita katika kesi tofauti walilipa faini ya jumla ya Sh.1,250,000/=. Mtuhumiwa wa kesi moja alihukumiwa miaka miwili bila yeye kuwepo Mahakamani, juhudi za kumsaka zinaendelea.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Serikali imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha maeneo ya uendeshaji na usimamizi wa rasilimali ya Menejimenti, Bodi, Mabaraza ya Madiwani, Ukaguzi wa Nje, Ukaguzi wa Ndani na kuliacha eneo muhimu la Kamati za Ukaguzi (Audit Committee) kwenye Wizara, Idara, Wakala na Serikali za Mitaa.
Je, ni lini Serikali itaboresha Kanuni ili muundo wa Kamati za Ukaguzi ziundwe na Wajumbe wengi (majority) toka nje ya taasisi kuzingatia weledi na uzoefu ili kusimamia rasilimali kwa tija na ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uanzishaji wa Kamati za Ukaguzi umetajwa katika Kanuni za Fedha za Umma za mwaka 2001 kama ilivyorekebishwa mwaka 2004 ambapo inaelezwa ya kwamba Kamati za Ukaguzi ziundwe na wajumbe watano; kati ya hao, mjumbe mmoja atoke nje ya taasisi. Aidha, kati ya wajumbe hao wa Kamati za Ukaguzi anatakiwa angalau mjumbe mmoja awe na uzoefu katika masuala ya uhasibu na ukaguzi wa hesabu.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, mwaka 2013 Wizara ya Fedha na Mipango ilitoa Mwongozo wa Utendaji Kazi wa Kamati za Ukaguzi katika taasisi za umma kuhusu idadi ya wajumbe kutoka nje ya taasisi kuwa wajumbe wawili au zaidi wateuliwe kutoka nje ya taasisi; mwongozo huo unawaelekeza Maafisa Masuuli kuwa wanaweza kuteua wajumbe kutoka nje ya taasisi kuanzia wajumbe wawili au zaidi. Hata hivyo, Wizara ya Fedha na Mipango inapitia upya Sheria ya Fedha za Umma na Kanuni zake ili tuweze kuwa na muundo mpya na huru wa Kamati za ukaguzi ili kuleta ufanisi.
MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na mauaji ya wazee na walemavu wa ngozi kutokana na sababu mbalimbali.
(a) Je, ni idadi ya watu wangapi waliopoteza maisha katika Jimbo la Ushetu kwa kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015?
(b) Je, mauaji ya makundi haya yanapungua au yanaongezeka katika Jimbo la Ushetu?
(c) Je, Serikali imeshirikisha vipi jamii kupiga vita mauaji haya, vikiwemo vikundi vya dini, walinzi wa jadi (sungusungu) na uongozi wa kimila Jimboni Ushetu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2010 wazee waliouawa walikuwa wawili, mwaka 2011 wazee wanne, mwaka 2013 wazee watano, mwaka 2014 wazee waliouawa walifikia sita, mwaka 2015 walikuwa wawili, mwaka 2016 wawili na mwaka 2017 alikuwa ni mzee moja. Kwa hiyo, jumla ya wazee ambao wamepoteza maisha katika kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwaka 2010 hadi 2017 ni wazee 22 katika Jimbo la Ushetu. Kwa upande wa walemavu wa ngozi, katika kipindi hicho hakuna mlemavu aliyeuawa wala kujeruhiwa Jimboni Ushetu ila kwa nchi nzima kwa kipindi cha miaka 2010 mpaka 2017 walemavu wa ngozi waliouawa walikuwa ni sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mauaji ya makundi haya katika miaka ya karibuni yanapungua kutokana na misako iliyofanywa ya kuwakamata waganga wa kienyeji ambao wanapiga ramli chonganishi na kuchochea imani za kishirikina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukomesha mauaji haya, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwemo kushirikiana na taasisi mbalimbali zisizo za Kiserikali ndani na nje ya Jimbo hilo katika kutoa elimu ya ukatili huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikishirikiana na jamii na taasisi za kidini, vikundi vya ulinzi jamii ndani na nje ya Jimbo la Ushetu kwa kuwapa elimu wananchi ili kudhibiti maujai hayo ya kikatili.