Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Stanslaus Haroon Nyongo (29 total)

MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-
• Je, Serikali kupitia REA III ina mpango gani wa kusambaza umeme katika kata zilizobaki Wilayani Nachingwea?
• Je, nini mpango wa Serikali kutatua tatizo la kukatikakatika kwa umeme Wilayani Nachingwea?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, nimshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa imani yake na nikushukuru wewe pia Mheshimiwa Spika kwa uongozi wako.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kuwa vijiji vyote visivyo na umeme vinapata umeme kupitia mradi kabambe wa kupeleka umeme vijijini Awamu ya Tatu (REA III) unaotegemewa kukamilika mwaka 2020/2021. Mradi huu utajumuisha vipengele vitatu vya Densification, Grid Extension na Off-Grid Renewables. Mkoa wa Lindi chini ya Mradi wa Uendelezaji wa Gridi mzunguko wa Kwanza unatekelezwa kwa muda wa miezi 24 na Kampuni ya State Grid & Technical Works Ltd. Katika Wilaya ya Nachingwea Mpango wa Awamu ya Tatu utavipatia umeme vijiji 30. Kazi za utekelezaji wa mradi zilianza mwezi Julai, 2017 na zitakamilika Juni 30, 2019. Aidha, vijiji vilivyobakia vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa REA III utakaoanza Aprili, 2019 hadi Disemba 2021.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme mzunguko wa kwanza itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 380, ufungaji wa transfoma 180, ujenzi wa njia za msongo wa kilovoti 0.4 zenye urefu wa kilometa 360 na uunganishaji wa wateja wapatao 5,710 katika Mkoa mzima wa Lindi. Aidha, kwa Wilaya ya Nachingwea jumla ya wateja wapatao 1,200 wataunganishwa. Mkandarasi anaendelea na upimaji wa njia za umeme ambapo amefikia asilimia 30 na kazi za upimaji zitakamilika mwishoni mwa Novemba, 2017. Gharama za miradi hiyo ni jumla ya shilingi 24,636,112,764.82 na dola za Kimarekani 5,657,471.30 pamoja na VAT.
(b) Mheshimiwa Spika, umeme unaotumika katika Wilaya ya Nachingwe unatoka katika kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia kilichopo Mtwara Mjini ambapo njia ya kusafirisha umeme kutoka Mtwara ina urefu wa kilometa 210 na pia hugawa umeme katika maeneo ya Mkoa wa Mtwara kabla ya kufika Nchingwea. Hivyo, pakitokea tatizo lolote mwanzoni au katikati ya njia basi, umeme hukatika katika maeneo mengi ya Mkoa wa Lindi, ikiwemo Nachingwea. Ili kukabiliana na tatizo hilo Serikali kupitia TANESCO imejenga njia mpya ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Mtwara hadi Mnazi Mmoja, Lindi na kujenga kituo cha kupoza umeme chenye uwezo wa MVA 20, 132/33kV ambapo ujenzi wake umekamilika na mradi mzima umegharimu jumla ya shilingi bilioni 16.
Mheshimiwa Spika, umeme utapozwa katika msongo wa kilovoti 33 na kusafirishwa kwenda katika Wilaya za Ruangwa, Nachingwea na badae Liwale. Ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 ya Wilaya ya Ruangwa unategemewa kuanza Januari, 2018 baada ya kupatikana kwa fedha za utekelezaji. Pamoja na ujenzi huo, ukarabati wa miundombinu iliyopo unaendelea ili kuboresha mfumo mzima wa usambazaji katika Wilaya ya nachingwea na Lindi kwa ujumla.
MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS NYIMBO aliuliza:-
Kuna taarifa zilizotolewa na Wizara ya Nishati na Madini za kugunduliwa kwa gesi ya Hellium yenye ujazo wa takribani futi bilioni 54 za ujazo nchini.
Je, Serikali imejiandaaje kimkakati kuhusu ugunduzi huo na uchimbaji wa gesi hiyo hasa ikizingatiwa kuwa mataifa makubwa kama Marekani yalishatangaza kukosekana kwa gesi hiyo ifikapo 2030?
NAIBU WAZIRI WA MADINI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos Nyimbo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Kampuni ya Hellium One Ltd. imegundua kiasi cha gesi ya Hellium yenye ujazo wa cubic feet 54 billions katika maeneo ya Ziwa Rukwa. Ugunduzi huo ulitokana na uchunguzi wa sampuli tazo za Mavujia yaani gas seeps ya gesi ya Hellium katika maeneo hayo kiasi ambacho kinakadiriwa kuwa kikubwa zaidi ya mara sita ya mahitaji ya dunia kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya Hellium One Ltd. imegundua madini ya hellium kupitia Kampuni zake tanzu za Gogota Tanzania Ltd., Njozi Tanzania Ltd. na Stahamili Tanzania Ltd. zinazomiliki leseni z utafutaji wa gesi ya hellium katika Mkoa wa Rukwa ikiwemo maeneo ya Ziwa Rukwa. Kampuni hizi zilipewa leseni za utafutaji wa hellium katika maeneo mbalimbali kuanzia mwaka 2015. Shughuli za utafutaji wa kina wa gesi ya helium unaendelea kwa kukusanya taarifa zaidi za kijiolojia, kijiokemia, kijiofizikia na 2D Seismic Survey ili zitumike kwa ajili ya uchorongaji wa visima vya utafiti yaani exploratoty wells. Kazi ya uchorongaji ikikamilika itawezesha kuhakiki kiasi halisi cha gesi ya hellium kilichopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji wa gesi ya hellium utaanza mara baada ya kazi ya utafiti wa kina, upembuzi yakinifu na tathmini ya athari za mazingira, kukamilika kwa leseni ya uchumbaji wa gesi hiyo kutolewa. Matokeo ya gesi hizo ndiyo yatakayoonyesha kama kiasi cha gesi kilichopo kinaweza kuchimbwa kibiashara kwa kipindi gani na taifa litanufaikaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kufundisha wataalam stahiki yaani wajiolojia, wahandisi wa migodi na wachumi wa madini kusudi wawe na ujuzi wa kutosha na hadi sasa Serikali ina jumla ya wataalam 454 wenye fani za mafuta na gesi katika viwango mbalimbali na elimu. Pia kuna wanafunzi 137 walipo katika mafunzo ya mafuta na gesi katika ngazi za shahada za uzamivu katika vyuo mbalimbali nje ya nchi na wanafunzi 455 katika ngazi ya diploma na shahada ya kwanza ndani ya nchi.
MHE. KISWAGA B. DESTERY (K.n.y. MHE. NJALU D. SILANGA) aliuliza:-
Maeneo mengi yamefanyiwa utafiti na kampuni za kigeni kwa muda mrefu bila kufikia hatua ya kufungua migodi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuzifutia leseni kampuni hizo na kuwapatia wachimbaji wadogo wadogo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza kabisa na mimi kwa sababu nimesimama hapa kwa mara yangu ya kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii kufika hapa leo. Vilevile nimshukuru pia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kuniamini na kuniweka katika Wizara hii mpya. Vilevile nimshukuru Mheshimiwa Spika, Wabunge wote na Wajumbe wa Kamati ya Viwanda na Biashara kwa malezi yao mazuri na kunifikisha hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Njalu Daudi Silanga lililoulizwa na Mheshimiwa Kiswaga ambaye ni Mbunge wa Magu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na kanuni zake inatambua umiliki wa leseni za utafutaji mkubwa wa madini na uchimbaji mdogo wa madini inayotolewa kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kama ilivyorekebishwa mwaka 2017, leseni za utafutaji wa madini aina ya metali, viwandani na nishati (makaa ya mawe na urani) hutolewa kwa muda wa miaka minne ya awali na kuhuishwa kwa mara ya kwanza kwa miaka mitatu na mara ya pili kwa miaka miwili. Hivyo leseni ya utafutaji mkubwa wa madini ya aina hizo hubaki hai kwa kipindi cha miaka tisa. Aidha, leseni za utafutaji wa madini na vito na ujenzi hutolewa kwa mwaka mmoja na haziwezi kuhuishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, iwapo mmiliki wa leseni atashindwa kuendesha shughuli za utafutaji wa madini, leseni yake hufutwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na Marekebisho yake ya mwaka 2017. Aidha, katika kipindi cha mwaka 2014/2015 hadi 2016/2017 jumla ya leseni 423 za utafutaji wa madini zilifutwa ambapo mwaka 2014/ 2015 zilifutwa leseni 2013, mwaka 2015/2016 zilifutwa leseni 155 na mwaka 2016/2017 zilifutwa leseni 65.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la leseni lililofutwa hutathminiwa na Wakala wa Jiolojia yaani Geological Survey of Tanzania (GST) kwa ajili ya kutengwa kwa wachimbaji wadogo endapo litaonekana kuwa na mashapo yenye tija. Katika kipindi cha mwaka 2014/2015 hadi 2016/2017 jumla ya maeneo 19 yenye ukubwa wa jumla takriban hekta 69,652.88 yalitengwa kwa wachimbaji wadogo katika maeneo mbalimbali nchini.
Aidha, Serikali itaendelea kufuatilia na kujadiliana na kampuni zilizomiliki leseni za utafutaji wa madini ili kuona uwezekano wa kuachia baadhi ya maeneo yanayofaa kwa uchimbaji mdogo.
MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-
Madini ya Tanzanite yanachimbwa Mkoani Manyara katika Wilaya ya Simanjiro, lakini madini hayo huchakatwa na kuuzwa Mkoani Arusha hali inayosababisha wananchi wa Manyara kutofaidika kiuchumi.
(a) Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu kujenga kiwanda cha kuchakata madini hayo Mkoani Manyara?
(b) Je, ni kiasi gani cha fedha kimeshachangiwa na madini haya katika mapato ya Mkoa wa Manyara?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Manyara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha kuwa madini ya Tanzanite yananufaisha wananchi wa Simanjiro, Serikali imetoa tamko la kutaka shughuli zote zinazohusu madini ya Tanzanite ikiwemo uendeshaji wa minada na ujenzi wa viwanda vya uchakataji wa madini hayo zifanyike katika eneo la Mererani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali imetenga eneo katika Kijiji cha Naisinyai, Mererani ili kuwa eneo maalum kiuchumi kwa ajili uanzishaji wa viwanda vya uchakataji (Economic Processing Zone - EPZ) ili kuvutia uwekezaji katika eneo hilo kwa kutoa vivutio mbalimbali kwa wawekezaji. Hivyo Wizara itaendelea kuhamasisha wawekezaji wa viwanda vya kuchakata madini ya Tanzanite kujenga viwanda katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza hilo kwa vitendo, Wizara ya Madini imepata kiwanja katika eneo la EPZ ili kujenga Kituo cha Umahiri (Center of Excellence), sehemu ya jengo hilo itakuwa na taasisi mbalimbali zinazosimamia shughuli za madini ili kutoa huduma kwa wafanyabiashara wa madini ya Tanzanite kwa haraka (One Stop Centre). Pia baadhi ya ofisi katika jengo hilo litatumika kutoa huduma za uthaminishaji wa madini na kuendesha minada.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2015 hadi 2017 madini ya Tanzanite yamechangia kiasi cha shilingi 140,954,229.37 kutokana na kodi ya tozo ya huduma (Service Levy) inayotozwa mujibu wa Sheria ya Ushuru wa Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, manufaa mengine yaliyopatikana kwa Wilaya ni pamoja na fursa za ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja kutokana na kuwepo kwa migodi katika eneo husika na huduma za jamii zinazotolewa na mgodi ambapo mgodi umetoa ajira kwa wafanyakazi 674 ambapo asilimia 93 ya walioajiriwa ni Watanzania na asilimia saba iliyobaki ni wageni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya waajiriwa hao, asilimia 21.81 ya wafanyakazi wameajiriwa katika vijiji kutoka vijiji vinavyozunguka mgodi vya Naisinyai na Mererani. Katika kipindi hicho mgodi wa Tanzanite One umefanikiwa kuchangia jumla ya dola za Kimarekani 429,664 katika utoaji wa huduma mbalimbali za kijamii ukilenga kuimarisha mahusiano na jamii zinazozunguka mgodi pamoja na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla. Huduma hizi zinahusisha masuala ya elimu, afya, lishe, ujenzi na sanaa.
MHE. EZEKIEL M. MAIGE aliuliza:-
Wananchi wa Msalala hususan wakazi wa Bulyanhulu wamefanyiwa dhuluma nyingi sana na Mgodi wa ACACIA, Bulyanhulu ikiwemo kuondolewa kwenye maeneo yao bila fidia mwaka 1996 na kwa wale wanaopata kazi mgodini kufukuzwa kazi bila kufuata utaratibu, kupata madhara makubwa ya kiafya na hata kusababishiwa vifo; na Serikali ya Awamu ya Tano imesimama kidete kutetea wananchi na kuwaepushia dhuluma hizi.
Je, ni hatua gani imefikiwa katika mazungumzo kati ya ACACIA na Serikali kuhusu ulipaji fidia kutokana na dhuluma hizo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mgodi wa Bulyanhulu unamilikiwa na Kampuni ya ACACIA na unaendelea shughuli zake za uchimbaji madini tangu mwaka 2000. Kabla ya kuanzishwa kwa mgodi huo fidia stahiki kwa ardhi ya wananchi iliyotwaliwa ililipwa. Kwa sasa mgodi hauna madai yoyote ya wananchi wa Bulyanhulu yatokanayo na fidia ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2007 wafanyakazi wapatao 1,331 wa Mgodi wa Bulyanhulu walifanya mgomo kinyume cha sheria hivyo wakaachishwa kazi. Hata hivyo wafanyakazi 643 walirudishwa kazini. Tarehe 6 Novemba, 2007 wafanyakazi 658 waliogoma kurudi kazini walifungua kesi mahakamani na kuomba kufanyiwa uchunguzi wa kiafya ili kubaini hali za afya zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uchunguzi huo wafanyakazi 78 walionekana kuwa na matatizo ya kiafya. Kwa sasa kampuni ya ACACIA inajadiliana na Serikali kupitia OSHA na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi kuhusiana na madai yao ya matibabu na fidia kulingana na sheria za nchi. Ili kupunguza magonjwa yanayohusiana na kazi za migodini Wizara inaendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu ili kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa kuzingatia usalama, afya mahali pa kazi, pamoja na utunzaji wa mazingira.
MHE. VICKY P. KAMATA aliuliza:-
Kampuni kubwa za uchimbaji madini kama vile GGM, Buzwagi Gold Mine na North Mara Gold Mine licha ya kulipa kodi kwa Serikali kuu pia zinawajibika kuhudumia jamii inayozunguka migodi kwa utaratibu wa uwajibikaji kwa jamii kwa kutoa fedha au kufadhili miradi ya kijamii au maendeleo:-
• Je, kwa mwaka 2017 Kampuni hizo kila moja ilitoa fedha kiasi gani?
• Je, hadi kufikia Januari mwaka 2018, Kampuni hizo zimetoa kiasi gani.
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda nijibu swali la Mheshimiwa Vicky Kamata, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kifungu cha 105(1) na (2) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017, kinamtaka mmiliki wa leseni kuandaa mpango wa mwaka wa utaratibu wa uwajibikaji kwa jamii (corporate social responsibility). Mpango huo lazima ukubalike kwa pamoja na Mamlaka ya Serikali ya Mtaa husika kwa kushauriana na Halmashauri ulipo mgodi kwa kuzingatia vipaumbele vya Halmashauri.
Mheshimiwa Spika, maandalizi ya mpango huo yanapaswa kumshirikisha Waziri wa Fedha na Mipango, Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kabla ya kuidhinishwa na Baraza la Madiwani la Halmashauri husika. Aidha, kila Halmashauri ulipo mgodi inapaswa kuandaa mwongozo wa uwajibikaji kwa jamii kwenye Halmashauri yao, kusimamia utekelezaji wake na kutoa elimu kwa wananchi wa Wilaya husika juu ya huduma hizo.
Mheshimiwa Spika, kwa takwimu zilizopo, migodi ya Geita Gold Mine, Buzwagi Gold Mine na North Mara Gold Mine imekuwa inatekeleza jukumu hili la kutoa huduma za jamii zinazozunguka migodi hiyo. Huduma ambazo zimekuwa zinatolewa ni kwa maeneo ya afya, elimu, maji, mazingira, ujasiriamali, miundombinu na jamii kama vile barabara, majengo na masuala ya sanaa na utamaduni.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2017, mgodi wa North Mara ulitumia dola za Marekani 1,837,495, sawa na takribani shilingi bilioni 4.25 kwenye huduma za jamii. Mgodi wa Buzwagi ulitumia dola za Kimarekani 595,658.47, sawa na shilingi bilioni 1.38 na mgodi wa Geita Gold Mine, dola za Kimarekani 6,358,542.24 sawa na shilingi bilioni 14.45.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kumekuwa na changamoto za gharama halisi za miradi hiyo. Kunaonekana ziko juu sana ukilinganisha na gharama halisi ya kile kilichotekelezwa. Marekebisho ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017 yaliyofanyika yanataka sasa Halmashauri zihusishwe katika kufanya maamuzi kuhusiana na mipango ya uwajibikaji kwa jamii.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018, migodi hiyo mitatu imekwishaandaa mpango kazi wa utekelezaji wa uwajibikaji kwa jamii. Maandalizi ya mpango yameshirikisha Serikali za Mitaa kama sheria inayowataka na kuwasilishwa kwa Halmashauri husika kwa ajili ya utekelezaji. Hadi kufikia Juni, 2018 mgodi wa Geita Gold Mine unatarajiwa kutumia kiasi cha dola za Kimarekani 1,932,142 na mgodi wa North Mara jumla ya dola za Kimarekani 333,111.39 na mgodi wa Buzwagi jumla ya Dola za Kimarekani 224,215.24
MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni kwa nini Serikali haiwapatii wananchi wa Mji wa Tunduma ruzuku ya asilimia 0.3 kama ilivyo kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye kuchimbwa madini?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, Mbunge wa Tunduma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 yaani Local Government Finance Act, Cap. 290, kifungu cha 6(1)(u), Halmashauri ulipo mgodi hutoza asilimia 0.3 ya mapato yote kabla ya kuondoa gharama za uzalishaji wa madini kama ushuru wa huduma yaani service levy. Aidha, kabla ya kuanza kutoza ushuru huo, Halmashauri husika inatakiwa kutunga Sheria Ndogo ya Halmashauri yaani District Council By-Laws ambazo zinaidhinishwa na Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa yaani TAMISEMI kwa mujibu wa kifungu cha 153(1) cha Mamlaka ya Serikali Mitaa yaani Local Government District Authority Act, Cap. 287.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, eneo la Halmashauri ya Tunduma hakuna leseni ya uchimbaji iliyotolewa. Hivyo, tunaendelea kuhimiza wawekezaji wa ndani na nje ili wawekeze katika utafiti na hatimaye kuanza kuchimba madini katika maeneo mbalimbali yenye madini nchini na Tunduma ikiwa mojawapo. Ahsante.
MHE. MARTHA M. MLATA – (K.n.y. MHE. JESCA D. KISHOA) aliuliza:-
Je, Serikali imejipangaje kuwatengea eneo la kuchimba madini katika Mgodi wa Shanta ulioko Mang’onyi (Singida), wachimbaji wadogo wadogo wa Wilaya ya Ikungi na Mkoa wa Singida wanaotegemea kupata kipato kwa shughuli hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nitoe pole kwa Mheshimiwa Jesca David Kishoa kwa ajali mbaya aliyoipata juzi na kupata maumivu, basi tumwombee kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kupata unafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo, naomba sasa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, nijibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya tarehe 10, Novemba, 2004 na tarehe 1, Aprili, 2005, wachimbaji wadogo wa madini wa Wilaya ya Ikungi waliwasilisha maombi 34 ya leseni ya uchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu katika eneo la Mang’onyi. Hata hivyo, maombi hayo yalikataliwa kutokana na kuombwa juu ya leseni ya utafutaji mkubwa wa madini yenye namba PL 2792/2004 ya Kampuni ya Shanta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kifungu cha 14(1) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017, kinaeleza kuwa mwombaji ambaye maombi yake yalipokelewa kwanza ndiye anayestahili kupewa leseni na hairuhusiwi leseni kutolewa juu ya leseni nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 7(2) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya mamlaka ya utoaji wa leseni, kwa ridhaa ya mmiliki wa leseni, inaweza kutoa leseni zaidi ya moja katika eneo moja la uchimbaji madini iwapo leseni inayoombwa ni ya madini tofauti na leseni iliyopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo mwezi Mei, 2014, Kampuni ya Shanta ilifanya mazungumzo na Kampuni ya Mang’onyi Company Limited ili iachie baadhi ya maeneo ya leseni inayomiliki na kukubali kutoa leseni tatu za uchimbaji wa madini ya dhahabu kwa wachimbaji wadogo wa Vijiji vya Sambaru, Mang’onyi na Mlumbi vilivyopo katika Kata ya Mang’onyi, Wilayani Ikungi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji hivyo vitatu vinazunguka leseni ya Mgodi wa Shanta. Pia kampuni ya Shanta imetoa kwa kikundi cha Aminika Gold Mining Co-operative Society Limited chenye wanachama 193 ambao ni moja ya wanufaika wa leseni hizo, kiasi cha dola za Marekani 25,000 kama fedha za mtaji wa kuendesha shughuli za uchimbani zilitolewa. Aidha, kampuni hiyo imepanga kutoa elimu ya usalama migodini ikifuatiwa na elimu ya uchimbaji ukiwemo uchorongaji wa miamba ili kuwezesha kikundi hicho kufanya shughuli za uchimbaji wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya mazungumzo na kampuni ya uchimbaji wa madini Shanta na kampuni hiyo imekubali kuachia eneo lote la leseni yake ya utafutaji mkubwa wa madini ya dhahabu iliyoko Muhintili Wilaya Ikungi yenye ukubwa takribani kilometa za mraba 71.3 ili itengwe kwa ajili ya uchimbaji mdogo wa madini. Kiasi cha leseni 714 zinatarajiwa kutolea kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa leseni 92 zimekwishatolewa kwa vikundi vya watu binafsi hivyo Wizara inawahimiza wachimbaji wadogo wa madini kuwasilisha maombi yao ili waweze kupatiwa maeneo ya uchimbaji. Hata hivyo, Serikali kupitia Wizara ya Madini itaendelea kutenga maeneo zaidi kwa ajili ya wachimbaji wadogo kwa madini kadri yanavyoweza kupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipekee niishukuru Taifa kubwa Simba Sports Club kwa ushindi walioupata, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MHE. AJALI R. AKBAR aliuliza:-
Madini aina ya Coltan yamegundulika katika Wilaya za Ruangwa, Masasi na Newala, lakini Wizara ya Madini imeweka beacon katika Kijiji cha Nandimba, Kata ya Chilagala.
(a) Je, ni utaratibu gani umetumika kuweka beacon katika Wilaya nyingine?
(b) Je, Serikali haioni kupora rasilimali ya wilaya nyingine kunaweza kusababisha migogoro?
(c) Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro huo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Akbar Ajali, Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini lenye sehemu (a), (b)na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Ruangwa, Masasi na Newala hakuna uthibitisho wa uwepo wa madini aina ya Coltan yaliyogunduliwa. Madini yaliyogunduliwa katika Wilaya hizo ni aina ya Graphite yaani madini ya Kinywe ambapo baadhi ya Kampuni zimepewa leseni za utafiti na uchimbaji wa madini hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017 na Kanuni zake, mmiliki wa leseni anatakiwa kuweka alama (beacon) zinazoonesha mipaka ya leseni yake ili jamii inayozunguka maeneo hayo ijue mwisho wa leseni husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, beacon zilizopo katika Kijiji cha Namlimba ziliwekwa na Kamuni ya Natural Resources Limited wakati wa ukusanyaji wa taarifa muhimu. Kampuni hii ya Natural Resources Limited ina umiliki wa leseni ya utafiti wa madini ya Graphite yenye nambari PL 10644/2015 ambayo mipaka yake inaingia kwenye Wilaya za Masasi na Newala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina lengo la kupora rasilimali ya Wilaya nyingine bali lengo lake ni kuhakikisha kuwa rasilimali madini zinazopatikana katika eneo husika, zinanufaisha wananchi wake na taifa kwa ujumla. Hadi sasa kampuni hiyo inaendelea na shughuli za utafiti wa madini ya graphite (kinywe). Pindi itakapogundulika uwepo wa mashapo ya kutosha, taratibu za kuvuna rasilimali hiyo kwa manufaa ya Watanzania wakiwemo wananchi wa Wilaya ya Newala zitafanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa Kampuni ya Natural Resources Limited haina mgogoro wowote na wananchi wa maeneo hayo. Namwomba Mheshimiwa Rashid Akbar Ajali kama kuna tatizo la mipaka ya kiutawala katika Wilaya za Masasi na Newala suala hilo liwasilishwe kwenye Wizara husika kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi.
MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA (K.n.y. MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA) aliuliza:-
Katika kutekeleza Mkataba wa Corporate Social Responsibility (CSR), Mgodi wa GGM unatumia bei za manunuzi kutoka nchi ya Afrika Kusini, mfano bei ya bati moja ni shilingi 81,000 na bei ya mfuko wa saruji ni shilingi 48,000.
Je, kwa nini Serikali isiziite pande hizi mbili, Mgodi wa GGM na Halmashauri ili iweze kumaliza mgogoro huo na kuweka utaratibu mzuri?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini kama lilivyoulizwa na Mheshimiwa Bukwimba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza matakwa ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017 kifungu cha 105, Halmashauri ya Mji wa Geita na Halmashauri ya Wilaya ya Geita pamoja na Mgodi wa Dhahabu wa GGM zimeandaa Mpango wa Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii wa mwaka 2018 (Corporate Social Responsibility Plan, 2018).
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuandaa mpango huo uliokuwa shirikishi, GGM iliwasilisha bei ya bati la geji 28 kwa kipimo cha mita za mraba ambapo bei ya mita moja ya mraba ilikuwa ni shilingi 81,000 na bei ya mfuko wa saruji ilikuwa ni shilingi 48,000 kwa mfuko mmoja. Aidha, baada ya bei hizo zilizopendekezwa na mgodi kuonekana kuwa ni kubwa, pande zote mbili ambazo ni Halmashauri ya Mji wa Geita na Halmashauri ya Wilaya ya Geita pamoja na Kampuni ya GGM walikaa na kufanya majadiliano ya pamoja na kukubaliana bei zilizopendekezwa na GGM zirekebishwe kwa kuweka bei ya bati moja na siyo bei ya bati kwa mita za mraba ambapo bati moja geji 28 ilikubalika kuwa shilingi 27,000 na mfuko mmoja wa saruji kuwa shilingi 18,000.
MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-
Wilaya ya Ileje imejaliwa kuwa na rasilimali ya makaa ya mawe ya Kiwira na Kabulo na STAMICO imekaririwa kuanza rasmi kuuza makaa hayo kwa kasi ili kukidhi mahitaji ya viwanda vya saruji na kukuza pato la Taifa, aidha, STAMICO ilianza uzalishaji wa majaribio ya makaa ya mawe katika Mgodi wa Kabulo tarehe 30/04/2017.
(a) Je, Mgodi wa Kabulo utaendelea kuchimba baada ya majaribio hayo na ni nani anayefanya uchimbaji huo?
(b) Je, kuna makubaliano gani na Wilaya ya Ileje juu ya mrahaba na uchumi kwa wana Ileje?
(c) Je, ni lini Mgodi wa Kiwira utaanza kufanya kazi na ni nini hasa kinachokwamisha?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la mama yangu, Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Jimbo la Ileje, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) lilianzishwa mwaka 1972 likiwa na jukumu la kushiriki na kusimamia maslahi ya Serikali katika sekta ya madini pamoja na rasilimali ya madini. Aidha, mwaka 2005 Mgodi wa Kiwira ulibinafsishwa kwa kampuni binafsi ya wazawa ya Tan Power Resources Ltd. (TPR) kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa umeme na kufikia megawati 200. Mnamo tarehe 30, Juni, 2014 Serikali iliikabidhi STAMICO Mgodi wa Kiwira kutokana na mbia mwenza kukosa mtaji wa kuendesha mgodi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, STAMICO ilianza uchimbaji wa majaribio katika leseni yake ya makaa ya mawe ya Kabulo mnamo mwezi Aprili, 2017 ambapo katika kazi hiyo jumla ya tani 8,674 za makaa ya mawe zilichimbwa. Baada ya kukamilisha majaribio ya awali STAMICO imeanza mchakato wa kumpata mkandarasi atakayefanya uchimbaji. Lengo ni mkandarasi huyo aanze kazi ya uchimbaji utakaozingatia taratibu zote za uchimbaji, mazingira na usalama mgodini katikati ya mwaka huu wa fedha yani 2018/ 2019.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, STAMICO kama ilivyo kwa wamiliki wengine wenye leseni za uchimbaji wa madini inawajibika kulipa ushuru wa huduma kwa Halmashauri wa asilimia 0.3 ya mapato ghafi yatokanayo na mauzo ya makaa ya mawe. STAMICO tayari imeanza kulipa ushuru wa huduma kwa Halmashauri ya Wilaya hiyo kutokana na mauzo ya makaa yaliyofanyika ambapo kiasi cha shilingi 57,600 kimelipwa. Aidha, jumla ya shilingi 1,735,900 zimelipwa kama ushuru wa barabara kwa Halmashauri. Manufaa mengine ni pamoja na kutoa ajira kwa wananchi wa Wilaya ya Ileje na kuchangia huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo afya, elimu na maji.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, STAMICO ilikabidhiwa Mgodi wa Kiwira mnamo mwezi Juni, 2014 ili kuendesha na kuusimamia kufuatia Kampuni ya Tan Power Resources kuurejesha Serikalini. Aidha, STAMICO imeendelea na jitihada mbalimbali za kutafuta fedha ikiwa ni pamoja na kutafuta wabia wenye uwezo watakaoshirikiana na shirika katika uendeshaji wa mradi huu.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-
Wawekezaji wanaotaka kuja kuwekeza kwenye Sekta ya Nishati na Madini wamepungua sana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita:-
(a) Je, ni nini kimesababisha hali hiyo?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha kuwa Wawekezaji wanaendelea kuja ili kukuza uwekezaji kutoka nje (Foreign Direct Investment] (FDI)?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, vichocheo vikuu vitatu vya uwekezaji katika Sekta ya Madini katika nchi yoyote, cha kwanza ni jiolojia inayoashiria uwezekano wa uwepo wa madini (prospective geology). Pili ni mwenendo wa bei ya madini husika kwenye Soko la Dunia na tatu Sera za Uchumi Mkuu (Macroeconomics) za nchi husika. Ilani ya CCM tunayoitekeleza hivi sasa ilizingatia vigezo hivi kwa kuhimiza kujenga uwezo wa Geological Survey of Tanzania ili waweze kugundua mashapo ya madini, kupunguza gharama za uzalishaji kwa kuboresha miundombinu na kuongeza thamani ya madini ili yawe na bei nzuri kwenye soko la dunia na kubadili Sheria ya Madini ili kuongeza uwazi na manufaa kiuchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha miaka mitano nchi yetu imeendelea kupokea wawekezaji kwenye sekta ya madini. Jumla ya leseni 102 za uchimbaji mkubwa (Special Mining Lenience) na wa kati (Mining License) zimetoelewa kati ya mwaka 2012/2013 hadi 2016/2017, ikiwa ni wastani wa leseni 20 kwa mwaka. Aidha, mwaka wa fedha 2012/2013 hadi 2016/2017 leseni 3,136 za utafutaji wa Madini (Prospecting License) zilitolewa, hii ikiwa ni wastani wa leseni 627 kwa mwaka. Mwaka 2017/2018, tumepokea maombi 26 ya Special Mining License na Mining License, yaani uchimbaji wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumepokea maombi 818 ya leseni za utafiti wa madini (Prospecting License). Tume ya Madini iliyoundwa hivi karibuni inaendelea kupitia maombi hayo na iwapo yatabainika kukidhi vigezo vya kisheria leseni hizi zitatolewa na hivyo kuendelea kuchangia kuongezeka kwa Foreign Direct Investment (FDI). Kwa takwimu hizi, bado wawekezaji wanaonesha nia ya dhati kuwekeza nchini kwani nchi yetu inakidhi sifa tatu nilizoainisha hapo awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuchukua hatua za makusudi kuandaa mazingira rafiki ya kuvutia wawekezaji na kutangaza fursa zilizopo nchini. Hatua zinazochukuliwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu wezeshi kama vile ujenzi wa barabara, reli, kupanua bandari, kujenga miundombinu, maji, umeme, gesi na mawasiliano kuelekea maeneo yanayotazamiwa kuanzishwa migodi. Aidha, Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) kwa kuwapatia wataalam vitendea kazi ili kuwawezesha kuongeza kasi ya kufanya tafiti za kina za maeneo yenye madini nchini. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:-
Je, ni lini Mgodi wa GGM utawasilisha bajeti yake ya kuhudumia jamii katika Baraza la Madiwani la Geita ili tuweze kuangalia kipaumbele chao na kuwapa vipaumbele vya Halmashauri ya Geita?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda sasa nijibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kifungu cha 105(1)(2) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na mabadiliko yake ya mwaka 2017 kinamtaka mmiliki wa leseni chini ya kifungu cha 7 cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 kuandaa Mpango wa Mwaka wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR). Mpango huo lazima ukubalike kwa pamoja na Mamlaka ya Serikali za Mtaa husika kwa kushauriana na Waziri anayehusika na Mamlaka za Serikali za Mitaa na Waziri anayehusika na Fedha.
Mheshimiwa Spika, mpango huo unapaswa kuzingatia masuala ya mazingira kijamii, kiuchumi na shughuli za tamaduni zilizopewa kipaumbele katika Mamlaka ya Serikali za Mtaa ya jamii inayozunguka mgodi.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa kifungu cha 105(3), mmiliki wa leseni anapaswa kuwasilisha kwa Mamlaka ya Serikali za Mtaa husika mpango huo aliouandaa kwa ajili ya kufanyiwa tathmini na kupata idhini kutoka kwa Baraza la Madiwani wa Halmashauri. Aidha, kila halmashauri uliopo mgodi inapaswa kuandaa mwongozo wa utoaji wa huduma kwa jamii kwenye Halmashauri yao, kusimamia utekelezaji wake na kutoa elimu kwa wananchi wa wilaya husika juu ya huduma hizo.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa Mgodi wa GGM, kwa kushirikiana na halmashauri mbili za Geita Mji na Wilaya ya Geita, umeweza kutekeleza mchakato wa kuandaa mpango wake wa kusaidia jamii (CSR) kwa mwaka 2018 kama sheria inavyotaka. Mchakato huo umehusisha wataalam kutoka halmashauri zote mbili na wataalam wa Sekretarieti ya Mkoa.
Mheshimiwa Spika, mpango wa miradi iliyotambuliwa na halmashauri hizo kama vipaumbele umeshawasilishwa kwenye Mgodi wa GGM na umesharidhiwa na mgodi. Mgodi wa GGM unatarajia kutumia takribani shilingi bilioni 9.124 katika kutekeleza miradi iliyo chini ya mpango wa CSR. Kiasi cha shilingi bilioni moja kitatumika kutekeleza miradi katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, takribani shilingi bilioni 6.824 zitatumika kutekeleza miradi katika Halmashauri ya Mji wa Geita na takribani shilingi bilioni 1.3 zitatumika kutekeleza miradi katika Halmashauri za Bukombe, Chato na Mbogwe.
Baada ya taratibu zote kukamilika, mpango huo utawasilishwa katika Baraza la Madiwani ili uweze kuidhinishwa. Miradi iliyokubaliwa na wadau wote kwa mwaka 2018 itaanza kutekelezwa kabla ya mwezi Juni, 2018.
MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-

Wachimbaji wadogo wadogo wa madini nchini wamekuwa wakipoteza maisha mara kwa mara kwenye mgodi:-

Je, ni lini Serikali itawapatia zana za kisasa pamoja na elimu ya kutosha wachimbaji hao?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum; kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhakikisha kwamba uchimbaji wa madini nchini unafuata taratibu za usalama, afya na utunzaji wa mazingira, Serikali imeanzisha Tume ya Madini ambayo ina Ofisi za Afisa Madini Wakaazi (RMO’s) takribani mikoa yote nchini. Vilevile kila eneo lenye shughuli za uchimbaji madini, Wizara imeanzisha Ofisi za Maafisa Migodi Wakaazi kwa lengo la kuimarisha shughuli za utoaji elimu kwa wachimbaji wadogo, ukaguzi wa migodi na ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachimbaji wengi katika migodi ya wachimbaji wadogo wamekuwa hawazingatii tahadhari za usalama wakati wa shughuli za za uchimbaji. Serikali itazidi kuweka msisitizo kwa wachimbaji wadogo kuzingatia Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017 na Kanuni zake za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira wakati wa uchimbaji. Aidha, Serikali haitasita kuyafunga maeneo yatakayobainika kuwa ni hatarishi na yanakiuka kanuni za usalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Madini ilikuwa ikitoa ruzuku kwa wachimbaji wadogo wa madini. Hata hivyo, ilibainika kuwa baadhi ya wachimbaji waliopatiwa ruzuku walitumia ruzuku hiyo kinyume cha maelekezo na makubaliano. Serikali inaanglia utaratibu mzuri wa kuwasaidia wachimbaji wadogo, ikiwa ni pamoja na kuzishawishi taasisi za fedha kuwakopesha wachimbaji wadogo. Wachimbaji wadogo wanashauriwa kutunza kumbukumbu za uzalishaji na mauzo ya madini ili kuzishawishi taasisi za fedha kuweza kuwakopesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE (K.n.y. MHE. AGNESS M. MARWA) aliuliza:-

Wananchi wengi walibomolewa nyumba zao na Mgodi wa ACACIA uliopo Nyamongo, Mkoani Tarime na wengine hawajalipwa fidia ya maeneo yao mpaka sasa. Aidha, Mgodi huo pia umeanza kuchimba chini ya ardhi ya maeneo ya watu (underground mining):-

Je, ni lini Mgodi wa ACACIA uliopo Nyamongo utalipa fidia kwa wananchi hao?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Agness Mathew Marwa ambalo limeulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kusimamia sekta ya madini kwa kuhakikisha uwekezaji unafanyika kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi ikiwemo kuhakikisha kuwa wananchi wanaoishi katika maeneo ambayo miradi na uendelezaji wa migodi inatake kufanyika na kulazimika kupisha maeneo yao wanalipwa fidia stahiki kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi na wanapewa makazi mbadala ambayo yana hali bora kuliko makazi waliyokuwa nayo awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uthaminishaji katika maeneo yanayozunguka Mgodi wa North Mara na ulipaji wa fidia umegawanyika katika awamu nyingi kwa kuzingatia vijiji husika kuridhia. Kijiji cha Nyabirama wakazi wake waliothaminiwa wote walilipwa fedha zao isipokuwa wakazi 138 ambao fidia yao iliyoidhinishwa ya shilingi bilioni 3 waliikataa na hundi zao zilitolewa na mgodi na ziko kwa Mkurugenzi wa Wilaya ya Tarime. Eneo la Kijiji cha Nyabichune lilithaminiwa katika awamu ya 47 lakini wananchi walikataa fidia husika iliyoidhinishwa. Aidha, eneo la Mrwambe lilithaminiwa katika awamu ya 30, 32, 32A na 32B na taarifa yake bado haijaridhiwa na Mthamini Mkuu wa Serikali. Taarifa hiyo ikisharidhiwa itawasilishwa kwa mwekezaji ili aweze kufidia wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Nyamichele ambacho nacho kina waathirika ambao wanatakiwa kufidiwa kuna changamoto ya uwepo wa taarifa mbili tofauti za uthaminishaji. Katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto hiyo, Wizara ya Madini kwa kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Mara tumekubaliana ifanyike tathmini mpya katika eneo hilo. Pia uthaminishaji utafanyika katika eneo tengefu la mita 200 (buffer zone 200 meters) lililotengwa kwa ajili ya uhifadhi wa maji ya kemikali na mabaki yanayotokana na shughuli ya uchenjuaji wa madini unaofanyika mgodini hapo. Kazi hii ikikamilika wahusika watalipwa stahiki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la mgodi kubadilisha aina ya uchimbaji kutoka uchimbaji wa wazi (open pit) kwenda kwenye uchimbaji wa chini (underground mining), uamuzi huo ulifanyika baada ya mgodi kufanya utafiti ulioonesha kuwa ilikuwa ni rahisi kutumia njia hiyo badala ya kuendelea na mgodi wa wazi. Niwatoe shaka wananchi wa Tarime kuwa Wizara yangu inafuatilia kwa karibu uchimbaji wa underground unaofanyika hivi leo. Uchimbaji huo unafanyika katika eneo la Gokona kuelekea Nyabigena ndani ya maeneo yao ya zamani ambayo walikuwa wameshachimba toka awali. Hivyo, hakuna eneo ambalo mgodi wa underground unachimba kwenye makazi ya wananchi.
MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:-

Wakazi wa Kitongoji cha Mafulungu kilichopo katika Kijiji cha Ilangali, Kata ya Manda wanajishuhgulisha na uchimbaji wa madini.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwawezesha wakazi hao ili shughuli zao za uchimbaji ziwe za ufanisi na zenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Livingstone Lusinde, Mbunge wa Mtera, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Manda, Kijiji cha Ilangali, Kitongoji cha Mafulungu, Wizara ilishatoa leseni 16 za wachimbaji wadogo wa madini ya jasi (gypsum) zilizotolewa kuanzia mwaka 2014 hadi 2016. Hadi sasa Tume ya Madini imepokea maombi 32 ya leseni za uchimbaji mdogo wa madini ya jasi kutoka katika eneo hilo. Maombi 16 yapo katika hatua za mwisho za kutolewa leseni na maombi 16 bado hayajakamilisha vigezo vya kupatiwa leseni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuwahamasisha wakazi wa Mafulungu kujishughulisha na uchimbaji wa madini sambamba na kutunza kumbukumbu za uzalishaji na mauzo ili waweze kuaminika na kukopeshwa na taasisi za fedha. Aidha, nawashauri wachangamkie fursa ya uwepo wa madini hayo katika kitongoji chao kwani mahitaji yake ni makubwa hasa katika viwanda vya saruji nchini na nchi za nje baada ya Serikali kuzuia uingizaji wa madini hayo kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Madini inaendelea kutoa elimu kwa wamiliki wa leseni kuhusu uchimbaji bora wa madini ya jasi na kuwataka kuchangia miradi ya maendeleo katika jamii kwenye maeneo yanayowazunguka katika migodi yaani kwa maana ya Corporate Social Responsibility kwani ni takwa la kisheria kama inavyoelekezwa katika kifungu cha 105 cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kama ilivyorekebishwa mwaka 2017.
MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA aliuliza:-

Katika Wilaya ya Kakonko kuna wachimbaji wadogo wa madini aina ya dhahabu katika Vijiji vya Myamwilonge, Nyakayenzi, Ruhuru na kuna dalili za kuwepo madini hayo katika sehemu nyingine. Aidha, kuna madini ya chokaa katika Milima ya Nkongogwa ambayo yana matumizi mengine ya viwandani:-

Je, Serikali imejipangaje kufanya utafiti wa uwepo wa madini na kuwasaidia wachimbaji ili wayachimbe na kujipatia kipato?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda sasa nijibu swali la Mheshimiwa Engineer Christopher Kajoro Chiza, Mbunge wa Buyungu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania ilifanya tafiti zifuatazo:-

(i) Upimaji na utafiti wa jiolojia uliofanyika mwaka 1960 na kuchora ramani ya jiolojia ya QDS (Quarter Degree Sheet) namba 43 pale Kakonko.

(ii) Utafiti wa pili ulifanyika mwaka 1978 – 1980 Serikali ilifanya utafiti wa jiofizikia kwa kutumia ndege na kufanya uchakataji wa takwimu zilizochukuliwa na hatimaye kuainisha maeneo yenye mipasuko ya miamba inayoashiria uwepo wa madini mbalimbali katika maeneo ya Kakonko na taarifa hizo zipo katika Ofisi ya GST (Geological Survey of Tanzania).

(iii) Utafiti wa tatu ulifanywa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ikiwemo Mradi wa Nordic Fund, Kampuni ya Beak Consultants ya Ujerumani na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kati ya mwaka 2003 na 2014 walifanya utafiti wa jiosayansi na kubainisha yafuatayo:-

(a) Uwepo wa madini ya dhahabu katika Kata ya Muhange, Kijiji cha Mwiluzi, Nyamtukuza, Nyamwilonge, Msekwa/ Galama, Kasela na Kata ya Kasuga katika Kijiji cha Nyakayenzi; na;

(b) Madini ya agate katika Kata za Kasanda, Kijiji cha Nkuba, Kata ya Gwanumpu katika Kijiji cha Kabingo na Kata ya Nyamtukuza katika Vijiji vya Nywamwilonge na Kasela.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia Geological Survey of Tanzania inakamilisha uandaaji wa kitabu cha madini yapatikanayo katika toleo la nne ambacho kinaonesha uwepo wa madini katika mikoa, wilaya na vijiji, hivyo kitasaidia wananchi na wachimbaji wadogo katika kutambua madini yaliyopo katika maeneo yao na matumizi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali kupitia Geological Survey of Tanzania itaendelea kufanya tafiti zaidi za kijiosayansi katika mwaka 2019/2020 kwenye maeneo ya Ruhuru na Nkongogwa katika Wilaya ya Kakonko ili kubaini madini yaliyopo katika maeneo hayo. Pia itatoa elimu kwa wachimbaji wadogo kuhusu njia bora za uchimbaji na uchenjuaji ili waweze kuelewa kuhusu jiolojia na madini yaliyopo kwenye maeneo yao na kuwashauri namna bora ya kufanya uchimbaji na uchenjuaji salama wenye tija kwa lengo la kuhakikisha kuwa wananchi wanafaidika na rasilimali ya madini iliyopo katika maeneo yao.
MHE. SELEMANI J. ZEDI (K.n.y. MHE. EZEKIEL M. MAIGE) aliuliza:-

Wananchi wa Msalala wengi wao ni wachimbaji wadogo, lakini hawana maeneo ya kufanyia kazi, maeneo mengi ya kufanyia kazi yana leseni za wachimbaji wakubwa na hawazifanyii kazi:-

(a) Je, kuna leseni ngapi za utafiti wa madini zilizotolewa kwa maeneo ya Halmashauri ya Wilaya ya Msalala?

(b) Je, ni maeneo gani Serikali inadhamiria kuyatoa kwa wachimbaji wadogo wa Msalala?

(c) Je, kwa kuanzia, Serikali inaweza kuwaruhusu wananchi wafanye uchimbaji mdogo kwenye maeneo ya reef 2, Kijiji cha Kakola namba Tisa, Kata ya Bulyanhulu, Bushimangila na Msabi Kata ya Mega na Lwabakanga na Nyangalata Kata za Lunguya na Bulyanhulu?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ya Hamashauri ya Wilaya ya Msalala kuna jumla ya leseni hai 78 za utafutaji madini na leseni za uchimbaji mdogo 53 zilizokwishatolewa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Halmashauri ya Msalala, Serikali imetenga eneo la Nyangalata lililopo katika Kata ya Lunguya lenye ukubwa wa kilometa za mraba 10.74 kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Hata hivyo, Serikali imedhamiria kutenga maeneo mengi zaidi katika Halmashauri ya Msalala, maeneo hayo ni Kata ya Segese maeneo mawili yenye ukubwa wa kilometa za mraba 19.67 na 9.84; Kata ya Mega lenye ukubwa wa kilometa za mraba 4.93; na Kata ya Kalole lenye ukubwa wa hekta 360.13.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haiwezi kuruhusu wachimbaji wadogo kufanya shughuli za uchimbaji katika maeneo ya Reef 2, Lwabakanga na Namba Tisa katika Kijiji cha Kakola, Kata Bulyanhulu kwa kuwa yamo ndani ya leseni ya uchimbaji mkubwa wa madini (special mining license) Na. 44/99 inayomilikiwa na Kampuni ya Bulyanhulu Gold Mine. Aidha, maeneo ya Bushimangila na Masabi yaliyopo katika Kata ya Mega yamo ndani ya maeneo yaliyoombewa leseni ya uchimbaji mdogo (primary mining license). Hivyo, natoa wito kwa wananchi wa Halmashauri ya Msalala kuchangamkia fursa katika maeneo yaliyotengwa na kupewa leseni ya uchimbaji mdogo ya Nyangalata.
MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-

Wananchi wa Kijiji cha Busiri, Wilayani Biharamulo ni miongoni mwa Watanzania ambao wanaendesha maisha kwa shughuli za uchimbaji mdogo kama ilivyo kwa wenzao wengi na kwingineko nchini. Uchimbaji mdogo wa Busiri unahitaji kuungwa mkono na Serikali kimkakati:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwaunga mkono wachimbaji wadogo wa Busiri na ni upi?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuwatembelea wananchi wa Kijiji cha Busiri ili kuwaelewesha ni namna gani itaanza utekelezaji wa mpango huo wa kuwaunga mkono wachimbaji hao?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, lenye vipengele
(a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali ina mikakati mingi ya kuwaunga mkono wachimbaji wadogo nchini wakiwemo wachimbaji wa Kijiji cha Busiri, Wilaya ya Biharamulo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mkakati wa kuwasadia wachimbaji wadogo nchini kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limenunua mtambo mkubwa wa kusaidia kufanya utafiti wa kina kwa kuchoronga miamba kwa bei nafuu ili kubaini mashapo zaidi na hivyo kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini inakamilisha uandaaji wa kitabu cha madini yapatikanayo Tanzania, toleo la nne, ambacho kinaonesha uwepo wa madini katika mikoa, wilaya, vijiji, hivyo kusaidia wananchi na wachimbaji wadogo ikiwemo wa Kijiji cha Busiri kutambua madini yaliyopo katika maeneo yao na matumizi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali za Madini (SMMRP), inakamilisha kujenga vituo vya umahiri katika Wilaya za Bukoba, Bariadi, Songea, Handeni, Musoma, Mpanda na Chunya ili kuwawezesha wachimbaji wadogo kujifunza kwa vitendo. Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa wachimbaji wadogo ili wanufaike zaidi na kazi ya uchimbaji.
MHE. PROSPER J. MBENA aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itafanya utafiti wa uhakika katika Vijiji vyote vya Jimbo la Morogoro Kusini ili kubaini madini yaliyopo?

(b) Je, Serikali itawasaidiaje Wachimbaji wadogo wa Rubi, Spinel na Dhahabu ili waweze kuzalisha zaidi na kupata masoko ya uhakika?

(c) Je, ni lini Serikali itatuma Wataalam wa kuthibitisha wingi wa madini ya Graphite na Chokaa katika maeneo ya Jimbo la Morogoro Kusini ili mipango ya kuchimba iweze kuanza?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Prosper Joseph Mbena, Mbunge wa Morogoro Kusini, lenye vipengele (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mwaka 2014, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) ilifanya utafiti wa awali wa kijiolojia katika Jimbo la Morogoro Kusini na kutengeneza ramani ya kijiolojia (Quarter Degree Sheet – QDS) zipatazo tisa.

Mheshimiwa Spika, taasisi kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ikiwemo kampuni ya Beak Consultants ya Ujerumani na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kati ya mwaka 2013 na 2014 walifanya utafiti wa awali na kubainisha uwepo wa madini ya dhahabu katika Kata za Mkuyuni, Mikese, Mazimbu, Kisemu na Tununguo; vilevile madini ya chokaa katika Kata ya Mkuyuni na Kisaki; madini ya Kinywe (graphite) katika Kata za Mvuha, Mkuyuni, Kisemu na Mtombozi.

Mheshimiwa Spika, aidha, utafiti huo ulibainisha pia uwepo wa madini ya ruby katika Kata za Tawa, Mkuyuni na Mkambalani. Vilevile kuna madini ya spinel na barite katika Kata za Mkuyuni.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali za Madini (SMMRP) imenunua mtambo wa kuchoronga miamba mipya na kuikabidhi katika Shirika la (STAMICO) kwa lengo la kufanya utafiti katika maeneo ya wachimbaji wadogo kwa gharama nafuu.
MHE. EDWIN M. SANNDA aliuliza:-

Uwepo wa madini ya chokaa umedhihirika katika Kijiji cha Ausia, Kata ya Suruke, Jimbo la Kondoa Mjini, kwa muda mrefu sasa, katika jitihada za kujaribu kunufaika wananchi wamekuwa wakichimba madini haya kienyeji:-

Je, ni lini Serikali itapeleka Wataalam kufanya utafiti kubaini kiwango cha uwepo na ubora wa madini hayo ya chokaa ili wananchi wa maeneo hayo waanze kunufaika sasa na rasilimali hiyo muhimu?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Mgante Sannda, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) hufanya utafiti wa awali wa madini (Regional Geological Mapping) na kuandaa ramani kupitia QDS yaani quarter degree sheet na taarifa za kijiolojia nchini. Utafiti huo wa awali husaidia kutangaza fursa za uwepo wa madini yanayogunduliwa ili wawekezaji binafsi wa madini wa nje ya nchi waweze kuwekeza katika tafiti za kina na uchimbaji. Hadi kufikia mwaka 1999, GST ilifanya utafiti wa Kijiolojia katika Wilaya ya Kondoa na kutengeneza Ramani za Kijiolojia yaani hizo QDS zipatazo sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo ikiwemo Kampuni ya Beak Consultants GmbH ya Ujerumani na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kati ya mwaka 2013 na 2014 ilifanya utafiti wa awali na kubainisha uwepo wa madini ya chokaa katika Vijiji vya Ausia na Tumbelwa, madini ya nickel katika Kijiji cha Ausia, madini ya dhahabu katika Vijiji vya Mpondi, Maji ya Shamba, Birise, Chang’aa, Jogolo, Tumbelo na Forya na madini ya shaba katika Kijiji cha Masange.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itazidi kuiwezesha GST na STAMICO kuendelea kufanya tafiti za kina kadri itakavyoweza kupata bajeti ya kutosha kama ilivyokwishafanya katika maeneo ya Tanga, Chunya, Katente, Mpanda, Kyerwa na Buhemba ili wananchi wanufaike na rasilimali za madini na kuwawezesha kuongeza kipato, kupunguza umaskini na kuongeza pato la Taifa kwa kulipa kodi stahiki.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-

Je, ni lini uzalishaji wa madini ya Niobium utaanza katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali, niungane na Watanzania wote kuwatakia kheri Waislam wote katika Mfungo wa Ramadhani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Uchimbaji wa Madini ya Niobium unaomilikiwa na Kampuni ya Panda Hill Mines Limited, kampuni hii ina ubia na kampuni ya Cradle Resources Limited asilimia 50 na Tremont Investment asilimia
50. Kampuni hiyo inamiliki leseni tatu za Uchimbaji wa Kati wa Madini Na.237, 237 na 239 za mwaka 2006 zilizotolewa tarehe 16 Novemba, 2006 zikiwa na jumla ya kilomita za eneo la mraba 22.1. Mradi utausisha uchimbaji wa madini ya Niobium ambayo yataongezewa thamani kwa kuchanganywa na madini ya chuma na kuwa Ferro-Niobium, zao ambalo litauzwa kwa wanunuzi mbalimbali walioko Ulaya, Asia na Amerika ya Kaskazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji ameshafanya upembuzi yakinifu (feasibility study) uliokamilka mwaka 2016 na kujiridhisha uwepo wa mashapo ya kutosha utakaowezesha uhai wa mgodi huo ambao utadumu kwa takribani miaka 30. Hata hivyo, kufuatia mabadiliko ya Sheria ya Madini ya Mwaka 2017, mwekezaji alilazimika kupitia upya na kurekebisha taarifa za upembuzi yakinifu ili kuzingatia viwango vipya vya mrabaha, kodi na hisa za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, mwekezaji amewasilisha andiko la mradi la kuomba ufafanuzi wa vipengele mbalimbali kwa sheria na kutoa mapendekezo yake juu ya utekelezaji wa mradi huo, pamoja na suala la fidia ya ardhi kwa Gereza la Mbeya ambalo linatakiwa kuhamishwa ili kupisha mradi huo. Baada ya kupokea andiko hilo, hatua mbalimbali zimechukuliwa ikiwemo majadiliano na mwekezaji ambapo Wizara inatarajia kutoa mapendekezo yatakayowezesha kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo.
MHE. ALEX R. GASHAZA aliuliza:-

Katika Jimbo la Ngara wapo wachimbaji wadogo wa madini ya Manganese katika Kata ya Murusagamba, Kijiji cha Magamba na tayari wamepata soko la madini hayo nje ya nchi ikiwemo India, Afrika Kusini na Uturuki:-

Je, Serikal iko tayari kutoa kibali kwa wachimbaji hao kuuza madini hayo yakiwa ghafi kutokana na kwamba hakuna mitambo ya uchenguaji hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Alex Raphael Gashaza, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imendelea kusimamia Sekta ya Madini kikamilifu kwa kuhakikisha shughuli za uchimbaji na biashara ya madini zinafanyika kwa kufuata sheria na taratibu za nchi ili rasilimali hiyo iweze kutoa mchango kwa Serikali kupitia malipo ya tozo stahiki za madini na pia itoe fursa ya ajira kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa Sekta ya Madini na kwa kuwa rasilimali hiyo siyo jadidifu (non renewable), mwaka 2017 ilifanya marekebisho ya Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na kutunga sheria mpya ya Mali na Urithi wa Asili (The Natural Wealth and Resources (Permanent Sovereignty) Act, 2017) ambayo imerasimisha umiliki wa rasilimali madini kwa Taifa. Kupitia sheria hizo, Serikali imetoa zuio la usafirishaji wa madini ghafi pamoja na makinikia nje ya nchi ili kuhamasisha uwekezaji katika tasnia ya uchenjuaji na uongezaji thamani wa madini nchini ambayo itatoa fursa ya ajira kwa Watanzaia na pia kutekeleza dhima ya Serikali ya kuwa na uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia changamoto inayowakabili wachimbaji wadogo wa madini ya viwandani yakiwemo madini ya manganese, Serikali inakamilisha utaratibu unaotumika katika kipindi cha mpito hasa kwa wachimbaji wadogo waliokuwa wamezalisha madini yao na kulipia tozo zote za Serikali kabla ya zuio hilo.
MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:-

Katika Jimbo la Nyang’hwale kuna maeneo mengi sana ya Wachimbaji wadogo wa madini ya Dhahabu kama vile Isakeli, Isonda, Lyulu, Nyamalapa, Lubando, Shibalanga na Kasubuya ambayo Wachimbaji hao wanafanya kazi na Dhahabu inapatikana bila utaratibu wowote?

(a) Je, ni lini Serikali itayarasimisha maeneo hayo na kuyagawa kwa Wachimbaji ili watambulike Kisheria na iwe rahisi kwa Serikali kukusanya kodi?

(b) Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake iliyoitoa mbele ya Waziri Mkuu ya kulitoa eneo la Bululu kwa Wachimbaji wadogo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar Mbunge wa Nyang‟wale lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Madini imedhamiria kuwaendeleza wachimbaji wadogo nchi nzima kwa kuwapatia maeneo ya uchimbaji ili waweze kuchangia uchumi kwa kulipa kodi, kujiajiri na kuongeza kipato cha Taifa.

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Nyanzaga Mining Co. Ltd iliyokuwa ikimiliki leseni ya utafiti Na. PL 9662 ya mwaka 2014 iliachia eneo lake lenye ukubwa wa eka 70 katika eneo la Bululu wilayani Nyang‟hwale. Aidha, eneo hilo limegawiwa kwa vikundi 22 vya uchimbaji wa madini ya dhahabu ambapo Tume ya Madini ilitoa leseni hizo tarehe 30 mwezi wa kumi na mbili mwaka 2019.

Mheshimiwa Spika, Eneo la Lubando lilikuwa na leseni ya uchimbaji wa kati wa Kampuni ya Busolwa Mining Co. Ltd. Hata hivyo, leseni hiyo ilifutwa na Serikali na kupewa wachimbaji wadogo. Aidha, eneo la Lyulu bado lina maombi ya leseni ya uchimbaji wa kati wa Kampuni ya Busolwa Mining Co. Ltd.

Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na Tume ya Madini inaendelea na juhudi zake za kutafuta maeneo mengine kwa ajili ya wachimbaji wadogo ambapo Tume ya Madini imewataka wamiliki wote wa leseni kubwa za utafiti kutimiza matakwa ya sheria vinginevyo maeneo yao yatafutwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na kupewa wachimbaji wadogo. Mwisho, Naomba kutoa wito kwa wamiliki wa leseni za utafiti wote nchini uchimbaji na wafanyabiashara wote wa madini kuendelea kuzingatia sheria za madini ikiwa ni pamoja na kuuza madini kwenye masoko yaliyofunguliwa nchini kote.
MHE. JANET Z. MBENE Aliuliza:-

Geological Surveys za Wilaya au Mikoa mingi ni za miaka mingi tangu enzi za ukoloni. Surveys hizi nyingi zimejikita kwenye aina moja ya migodi kwa mfano Mkoa wa Songwe Survey imezungumzia machimbo ya mawe peke yake:-

(a) Je, ni lini Serikali itafanya mapitio ili kupata Geological Surveys zenye kujumuisha aina nyingine za madini ambayo yanapatikana katika Mkoa wa Songwe hususan Ileje?

(b) Je, Serikali ipo tayari kwenda kuwaelimisha wananchi wa Ileje juu ya madini yaliyopo na kuhamasisha uwekezaji kwa wachimbaji wadogo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, Mbunge wa Ileje, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imekuwa ikifanya tafiti mbalimbali za jiolojia kwa ajili ya kuainisha madini mbalimbali yaliyopo nchini tangu kipindi cha mkoloni hadi sasa. Aidha, GST kwa ushirikiano na ufadhili wa Serikali ya Jamhuri ya watu wa Korea imeanza kufanya utafiti wa kina wa kijiolojia ili kuongeza na kuboresha taarifa za uwepo wa madini mengine katika Mkoa wa Songwe na mikoa mingine nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti zilizofanyika Mkoa wa Songwe zinaonesha kuwa Wilaya ya Ileje ina madini yafuatayo; moja ikiwa ni madini ya metali aina ya dhahabu yanayopatikana katika maeneo ya Mwalisi na Ikinga, Madini ya Viwandani aina ya Ulanga, yanayopatikana katika maeneo ya vilima vya Bundali na Ileje, madini ya nishati aina ya makaa ya mawe (Coal) yanapatikana katika maeneo ya Songwe, Kiwira na madini ya apatite na niobium yanayopatikana katika miamba ya carbonatite iliyopo maeneo ya kilima cha Nachendazwaya, ikiwa ni pamoja na madini mengine kama marble na madini mengine ya ujenzi.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania itaendelea kufanya tafiti mbalimbali za madini katika Wilaya ya Ileje na maeneo mengine ya nchi kwa kadri ya upatikanaji wa rasilimali ya fedha na kutoa elimu kwa wananchi juu ya upatikanaji wa madini katika maeneo mbalimbali ya nchi ikiwa ni pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya madini kwa wachimbaji wadogo.
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-

Sekta ya Madini inaongeza pato kubwa katika uchumi wa nchi.

Je, Serikali iko tayari kutatua kero kwa wachimbaji wadogo na vibarua ambao wananyanyasika katika migodi mbalimbali hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Wizara kupitia Tume ya Madini imeendelea kuweka mikakati ya kuwatambua wachimbaji wadogo kwa kuwapatia leseni za uchimbaji. Aidha, Wizara ya Madini imeendelea kuhamasisha watanzania kote nchini kujiunga latika vikundi kwa mujibu wa sheria ya vyama vya ushirika, ili waweze kupatiwa elimu kiurahisi kuhusu uchimbaji salama, utunzaji wa kumbukumbu na uzalishaji na namna ya kupata mikopo kwa riba nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wizara imedhamilia kuondoa kero za wachimbaji wadogo hasa za maeneo ya kuchimba ili kuwawezesha kujiajiri katika sekta ya madini. Aidha, nimeagiza Tume ya Madini kuhakikisha wamiliki wote wa leseni za utafiti ambazo hazifanyiwi kazi zifutwe ili maeneo hayo yamilikishwe wachimbaji wadogo wenye lengo la kuviendeleza ili kuongeza mchango kwa sekta ya madini katika pato la Taifa na kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migodi yote hapa nchini, inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na marekebisho yake ya Mwaka 2017 na kuzingatia kanuni za uchimbaji salama, mazingira na afya kwa wafanyakazi. Suala la unyanyasaji wa aina yoyote halikubaliki na mmiliki anayefanya hivyo atakuwa anavunja Sheria ya Madini na Sheria za Kazi Mahali pa Kazi. Aidha, natoa wito, kwa yeyote mwenye malalamiko ya msingi kutoa taarifa kupita ofisi za madini zilizoko mikoani mwao ili yaweze kushughulikiwa kwa mujibu wa sheria.
MHE. UPENDO F. PENEZA aliuliza:-

Wananchi wa Mtaa wa Mgusu wanaoishi ndani ya mipaka ya Mgodi wa Geita Gold Mine wanaathirika sana na uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka zinazomwagwa katika maeneo karibu na wananchi.

Je, ni lini Serikali itatoa agizo kwa Geita Gold Mine kulipa wananchi fidia ili watoke katika eneo lililomilikishwa Mgodi?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini naomba nijibu swali la Mheshimiwa Upendo Furaha Peneza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nijibu kama swali lilivyoulizwa na kama ni marekebisho hayo anayoyasema Mheshimiwa Mbunge basi tunaomba arudishe swali alete jingine jipya tutamjibu kwa lile eneo lakini hapa tumemjibu kadri lilivyoulizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mtaa wa Mgusu uko kilomita 4.5 kutoka eneo la uchimbaji la Nyamulilima Star and Comment la GGM ambapo kwa sasa uchimbaji unaendeshwa kwa niia ya chini kwa chini yaani Underground Mining Operations. Mawe ya Dhahabu yanayozalishwa katika eneo hilo hupelekwa kwenye eneo maalum la uchenjuaji yaani Processing plant ambalo lipo umbali wa kilomita 19 kutoka Mtaa wa Mgusu. Kwa umbali huo ni wazi kuwa ni vigumu kwa taka ngumu kufika katika Mtaa huo. Hata hivyo ukingo wa miamba isiyo na madini yaani Waste Rocks umewekwa ili kuzuia miamba hiyo kutoka nje ya eneo la uchimbaji.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, Kifungu cha 96(1) na 97(1)(a) na (b) vinaeleza kuwa, fidia inapaswa kulipwa kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi katika hatua ambapo muwekezaji anataka kuanza kuchimba madini baada ya kushauriana na Mamlaka ya Serikali za Mtaa husika na kujiridhisha juu ya madhara yanayoweza kusababishwa na uchimbaji huo.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mtaa wa Mgusu wengi wao wanajishughulisha na uchimbaji mdogo wa madini. Hata hivyo tathimini ya mazingira iliyofanywa na mgodi wa GGM haionyeshi uwepo wa madhara yanayohitaji kuhamishwa kwa wananchi wa Kitongoji hicho. Aidha, Wizara kupitia Ofisi ya Madini Mkoa wa Geita itaendelea kusimamia na kukagua eneo hilo.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-

Serikali ilituma wataalam wa madini, mazingira na maji katika Kijiji cha Sakale, Tarafa ya Amani kuangalia uwezekano kama uchimbaji wa dhahabu unawezekana katika maeneo hayo.

Je, Serikali imefikia uamuzi gani kuhusu suala hilo?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 02/10/2018 timu ya wataalam wa madini, mazingira na maji kutoka Ofisi ya Tume ya Madini Tanga, Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, wataalam wa Bonde la Mto Zigi, Maafisa Misitu na Serikali ya Kijiji walitembelea na kukagua eneo la Kijiji cha Sakale na Kiara ili kuangalia athari za uchimbaji uliokuwa unafanywa na wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya ukaguzi, timu ya wataalam ilibaini uharibifu mkubwa wa mazingira uliofanywa katika vyanzo vya maji na Msitu wa Amani na hivyo shughuli za uchimbaji madini zilisitishwa katika eneo hilo ili kunusuru mazingira, vyanzo vya maji na Msitu wa Amani. Katika kusaidia utunzaji wa mazingira, Mradi wa Matumizi Endelevu ya Ardhi katika Bonde la Mto Zigi unaendelea na unafadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Kimataifa (UNDP) kwa kushirikiana na Wizara ya Maji kwa manufaa ya sasa kwa wananchi na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa wito kwa wachimbaji wadogo wa Tarafa ya Amani kuangalia maeneo mengine nje ya Bonde la Mto Zigi ili kufanya shughuli za uchimbaji.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-

Kampuni ya Mabangu ina leseni ya utafiti wa madini katika maeneo ya Nyakafuru, Bukandwe na Kanegere Wilayani Mbogwe; kampuni hiyo inafanya utafiti kwa kushirikiana na kampuni nyingine ya Resolute lakini utafiti huo umechukua muda mrefu.

(a) Je, ni lini kampuni hizo zitafungua mgodi katika eneo lao la utafiti?

(b) Kama kampuni hizo zimeshindwa kuanzisha mgodi; je, Serikali iko tayari kuona uwezekano wa kuligawa eneo hilo kwa wachimbaji wadogo wa Wilaya ya Mbogwe?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Augustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya Nyakafuru, Bukandwe na Kanegere katika Wilaya ya Mbogwe yana leseni ya utafiti mkubwa yenye ukubwa wa kilometa za mraba 17.53 inayomilikiwa na Kampuni ya Mabangu Mining Limited ambayo ni kampuni tanzu ya Resolute Tanzania Limited kupitia leseni ya utafutaji wa madini namba PL 5374/2008. Leseni hiyo ilitolewa kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 1998 tarehe 24/10/2008 kwa kipindi cha miaka tatu ya awali.

Aidha, kulingana na Sheria ya Madini ya mwaka 2010, leseni hiyo ilihuishwa kwa mara ya kwanza kwa kipindi cha miaka mitatu na mara ya pili kwa miaka miwili.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile mwaka 2016 kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, leseni hiyo iliongezewa muda (extension) kwa kipindi cha miaka miwili ili kukamilisha kazi ya upembuzi yakinifu kabla ya kuwasilisha maombi ya leseni ya uchimbaji na hivyo leseni hiyo kumaliza muda wake tarehe 23/10/2018. Kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka 2017 eneo la leseni hiyo limerudishwa Serikalini baada ya kumaliza muda wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, mgodi katika eneo la Nyakafuru Wilayani Mbogwe utafunguliwa baada ya kampuni yaMabangu Mining Limited kuomba leseni ya uchimbaji wa madini kwa mujibu wa sheria na endapo Serikali itaridhia maombi hao, leseni itatolewa na shughuli inaweza kuanza, ahsante.