Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jumanne Kibera Kishimba (32 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii kuchangia bajeti hii ya Serikali ya Awamu ya Tano ya 2016/2017. Kwanza napenda kukupongeza wewe mwenyewe Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Fedha, Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa ndani ya Bunge hili. Vile vile napenda kutoa shukrani nyingi kwa wapigakura wangu wa Jimbo la Kahama kwa kunipatia kura nyingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita sehemu moja ya kuongeza mapato. Ni sehemu ngumu kidogo, lakini naomba nichangie na naomba Waziri wa Fedha kama anaweza kunisikiliza ni vizuri akanisikiliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ya Tanzania imezungukwa na nchi nyingi ambazo zina madini na maliasili nyingi na nchi hizi zinategemea nchi yetu ya Tanzania kupitishia madini haya na maliasili hizi. Vile vile zinategemea kuuza nchi za nje kupitia hapa kwetu. Ninachoomba kwa Waziri wa Fedha, kama anaweza kutukubalia, nitatoa mfano wa nchi ya Burundi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi ya Burundi imekuwa iki-export dhahabu tani tatu mpaka tani nne kwa utafiti unaoonesha, lakini nchi hii ina migogoro mingi ya vita na haina machimbo au mgodi wowote wa dhahabu, lakini sisi nchi yetu ina amani, ina dhahabu nyingi, imezungukwa na nchi nyingi kama Congo, Mozambique; nchi hizi zote zinataka kuuza madini yao hapa. Kuna madini ya almasi, nickel, copper, aluminium na madini zaidi ya 50.
Mheshimiwa Naibu Spika, na madini haya sisi si watumiaji. Tungeomba kwenye bajeti hii, kwa kuwa haiingiliani na bajeti hii, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama atakubali yaruhusiwe yawe zero wakati wa ku-export yawe one percent. Kwa hesabu ya harakaharaka Tanzania inaweza kupata kwa wiki tani mbili na nusu za dhahabu, maana yake kwa mwezi tutapata tani kumi na mbili na nusu zikiwa za sisi nyumbani na za watu wa nje. Kama tuta-charge kwa one percent kwa bei ya leo ya Dola 40 kwa gram au Dola 40,000 kwa kilo, tutapata zaidi ya Dola milioni 500. Dola milioni 500 kwa exchange ya harakaharaka ni trilioni moja kwa mwezi, hiyo ni kwa madini ya aina moja. Tukichukua madini mengine haya yaliyobaki yanaweza kutuchangia zaidi ya bilioni 900 kwa mwezi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukichukua one percent pia kwenye hiyo tutakuwa karibu tuna bilioni tisa kwa mwezi. Kwa hiyo, total itakuwa na bilioni 20 kwa mwezi na pesa hii haiingiliani na Bajeti ya Serikali, ni pesa ambayo ipo tukikataa au tukikubali yenyewe iko vile vile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, attendance ya watu hawa wakija kuuza madini lazima asilimia 20 ya pesa zao wafanye shopping hapa. Kama watafanya shopping asilimia 20, maana yake watatuachia sisi bilioni 400. Bilioni 400 maana yake tutakua sisi kwa asilimia 18 ya VAT ya vitu vilivyoingia nchini ambavyo watanunua hapa, Serikali itakuwa imepata bilioni 40 tena zaidi. Kwa hiyo, madini haya yatakuwa yametuchangia zaidi ya bilioni 70 kwa mwezi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna mahali ambapo Bajeti ya Serikali itakuwa imeguswa. Ni kiasi cha Waziri wa Fedha kusema kesho kwamba, sawa amekubali na watu hawa wanaanza kupita. Maana yake hata bila kukubali au namna gani hawa watu wanaendelea kupita hapa, wanahangaika kutoka hapa mpaka Dubai kwenda kuuza; kutoka Congo mpaka Dubai ni karibu masaa tisa, lakini kuja hapa ni masaa mawili. Kwa hiyo ingekuwa vizuri Waziri wa Fedha akaliangalia sana suala hili. Suala hili ndio utajiri wa hawa tunaowaomba pesa leo na ndio wanaotunyanyasa, lakini pesa zote zimetokana na njia hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, madini haya, sisi hatuyatumii, yanakwenda yote Ubeligiji, yanakwenda Dubai, yanakwenda Singapore, yanakwenda China, yanakwenda Hong Kong na mwisho wake sisi tunakwenda kuwaomba pesa wao. Ingekuwa vizuri, tukarekebisha sera yetu ili madini haya yaweze kutusaidia sisi hapa na jirani zetu waweze kugeuza hapa kuwa Dubai ya kwao.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote, kwa madini haya tutapata wageni zaidi ya 10,000 kwa mwezi. Wageni hawa ni wageni ambao wana pesa, maana yake hakuna mtu anayebeba madini akiwa hana pesa! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatarajia Sekta zote zitapata pesa kuanzia Usafirishaji, TRA, Uhamiaji, maduka, nyumba za kulala wageni, zote zitapata pesa na itatusaidia vile vile, kutuongezea na kutufungulia mlango mpya wa biashara ambao sisi hatukuwa nao. Sisi tumeelekeza zaidi kwenye utalii na nafikiri huu unaweza kuwa ni utalii mpya. Kwa namna hiyo, inaweza ikamsaidia Waziri wa Fedha akawarudishia na Wabunge pesa tunazozozana hapa za posho kama ataweza kukubaliana na wazo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo mchango wangu ni huo, asante sana na naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwanza na mimi naungana na Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake nzima kwa bajeti hii aliyotuletea. (Makofi)

Mimi nina suala moja tu la afya; ugonjwa siyo kitu ambacho unaweza kuchagua wala kupanga muda wa kuugua wala uwe na pesa kiasi gani au uwe maskini. Ni kweli kabisa napongeza Serikali hasa vijijini dawa ni nyingi sana sana kwa mara ya kwanza toka mwaka 1980 kumeonekana dawa nyingi sana sana hospitalini hata mimi mwenyewe nashangaa na tunashukuru sana kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa sana aliyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye afya bado kuna matatizo mawili au matatu; tatizo la kwanza sisi tunaotoka mikoa ya Kanda ya Ziwa ambako wenyeji wa maeneo yale aidha, hawataki kukata bima kwa ajili ya tradition yao kwamba watakuwa wanajitabiria kifo au kujitabiria ugonjwa, tunaomba Wizara ya Afya au TAMISEMI wawaruhusu wanakijiji wetu anapokuwa ameugua kama ana mbuzi au kuku hospitali au zahanati zetu zipokee atibiwe ili asubuhi au mchana ziuzwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivi mtu ameugua mchana au usiku yeye hana pesa lakini anatakiwa aende hospitali na bima hana na leo kuuza mfugo ni kazi lakini kama atapokelewa mfugo au mahindi, atapata matibabu na kesho yake vitu hivyo vitauzwa, hakuna daktari ambaye hajui kuku wala nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wetu ni maskini, sasa hivi kumezuka kwenye hospitali za Serikali na za Misheni kitu cha kusikitisha sana. Mtu anapokufa kwanza unapewa bill ya marehemu ukiwa huna pesa wanakatalia maiti na maiti ile wanaenda kuizika kama wanatupa mbwa, ni kitu kibaya sana na humu ndani nashangaa Mheshimiwa Waziri Mpango sisi wote ni maiti watarajiwa, Bunge zima.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kishimba naomba ukae kidogo, Waheshimiwa Wabunge kwa mujibu wa Kanuni ya 28(5) naongeza muda wa nusu saa ili Mheshimiwa Kishimba aweze kumaliza mchango wake. (Makofi)

MHE.JUMANNE K. KISHIMBA:Ahsante sana Mheshimiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena kwamba humu ndani wote Waheshimiwa Wabunge sisi ni maiti watarajiwa kasoro itakuwa muda, tarehe na wakati. Ni kweli ukiangalia kwenye bajeti yetu tumesamehe unga wa keki, lakini tunatoza tozo la maiti kwenye mortuary nakuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha au Naibu Waziri wa Fedha hebu rudisha hiyo kodi ya unga wa keki ili tufute tozo la maiti kwenye mortuary. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 95 ya vifo vinatokana na kuumwa na kuumwa kwenye mara nyingi ni kwa muda mrefu, kunapokuwa kwa muda mrefu huyu mtu anakuwa amedhoofika kiuchumi, amedhoofika kiafya sasa leo anafariki ni kweli hospitali inampa bili ya shilingi 500,000 anazipata wapi ameshakufa na huyu mtu wachangiaji wengi humu wamesema Watanzania woote wanalipa kodi wanavuta sigara, wanakunywa bia, wanafanya shughuli zote, sasa kwa nini Serikali isimsamehe mtu aliyefariki imsamehe bili halafu hizo pesa tuzipeleke kwenye keki ni hatari sana watengeneza bajeti najua ni vijana wetu wa Oysterbay ambao nafikiri walijua keki ni kitu cha muhimu sana ndiyo maana wakashindwa kuelewa kwamba kuna shida nyingi sana kule kwetu vijijini. (KIcheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ulikuwa Kahama juzi nashukuru sana umepita mle njiani zile nyumba unaziona mle za nyasi ni waganga wa kienyeji. Waganga wa kienyeji ukipeleka mgonjwa bahati mbaya akafariki hawaombi pesa badala yake wanakusaidia na sanda, inawezekanaje sisi Serikali tumdai mtu aliyefariki halafu tukatalie maiti, halafu maiti tukaizike kwa kutupa kwa gharama na bahati nzuri Mheshimiwa Msigwa ni Mchungaji na Mama Lwakatare wangetusaidia sana maana yake turuhusiwe basi watu wakafanye maombi kule kwenye makaburi ya Serikali wajue na kaburi ya ndugu yao ili baadaye baada ya miaka 10 watoto wakipata hela wakachukue mifupa ya baba yao au mzazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kitu ambacho kweli ni vizuri tukiangalie sana kama watakubali ni vizuri sana warudishe kodi ya keki maana yake hapo wamefuta kodi ya unga wa keki wanasema unga wa ngano ambao unatengeneza vyakula, vyakula gani ni keki na biskuti. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo la pili hapa sasa hivi kumezuka mtindo huu wa x-ray na dialysis ya figo. Daladala inauzwa shilingi milioni 50 mpaka shilingi milioni 100 kwa siku inaleta shilingi 50,000 mashine ya x-ray inauzwa shilingi milioni 40 mpaka shilingi milioni 100 na yenyewe mashine zote hizi, kwa nini hii inafanya shilingi 200,000 au shilingi 40,000 kwa mtu mmoja kwa nini Serikali isiruhusu watu wanunue x-ray wazipeleke hospitali ili bei ya hizi x-ray ipungue? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua wataalamu wataleta maneno mengi sana ambayo yanahusu afya, yanahusu nini lakini ni uongo, ni uongo kwa sababu waganga wa kienyeji wanapewa kibali na Wizara ya Afya kuendesha shughuli zao na waganga wa kienyeji hawana elimu yoyote ya hospitali, kule kwetu Kanda ya Ziwa mgonjwa mahututi ndiyo anapelekwa kwa mganga wa kienyeji ambako hakuna choo, hakuna kitu chochote, ni vipi Serikali ikatae leo kuwa watu wanunue wapeleke hizo x-ray kwenye hospitali ili bei hii ipungue? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa watu wetu ambao ni wa mjini ambao hawana pesa, nchi nyingi sasa hivi duniani bili yako ya maji na bili ya umeme inakudhamini hospitali. Anapofika mtu akatibiwa ikija bill ni shilingi 24,000 mnakaa na hospitali mna-bargain kwamba utalipa shilingi 4,000, 4,000 wanakwambia lete bill yako ya maji au bill ya umeme wanaingiza shilingi 4,000, 4,000 mle kwa kuwa TANESCO na Idara ya Maji ni taasisi za Serikali, wakichukua ile shilingi 4,000 wataipelekea hospitali, lakini mtu wetu anakuwa amepona kuliko sasa hivi kama huna pesa ni tatizo sana sana, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha aliangalie sana suala hili ili kusudi itusaidie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea suala zima la biashara; juzi kwenye mkutano wa Mheshimiwa Rais suala walilokuwa wanalalamika karibu wafanyabiashara wote lilikuwa ni suala la investigation baada ya kuwa mtu umemaliza kulipa kodi. Suala la kutafuta watu watakatifu mimi siliamini maana yake dini ina zaidi ya miaka 2000 toka Bwana Yesu aje, lakini mpaka leo watu hawajashika dini, dawa ya kumaliza mgogoro ni kuondoa zile sheria ambazo zinatusababishia mgogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, TRA wanayo sheria inayoruhusu mtu ambaye hakufanya hesabu wam-charge kwa percent ya mauzo, lakini sheria ile inawaruhusu wao kumu-investigate yeye, lakini sheria ile iliachwa na mkoloni na ilikuwa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwamba kama mtu hana vitabu atalipa 2% ya mauzo yake, lakini na yeye asilete gharama zake, kwa hiyo kama mtu ameuza shilingi bilioni moja, analipa shilingi 20,000,000 na yeye hawezi kuleta hesabu zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu asilimia 90 ya wafanyabiashara wa Tanzania elimu yetu ni darasa la saba, wengine hawakusoma kabisa. Sasa inakupa kazi ngumu sana utunze store ya mali, utunze na stoo ya karatasi na bado karatasi hizo ukizipeleka unaambiwa hazifai lazima utatoa hela. Lakini kama wao TRA walishamfanyia investigation mtu zaidi ya miaka mitano, wakajua huyu mtu sells zake huwa ni hizi na tulikusanya hela hizi kwa nini wasichukue formula ile ile wakaigawa ikaenda kwenye sells ya mauzo ambayo itamaliza kabisa ule ugomvi wote uliokuwepo siku ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni suala la Kariakoo; ni kweli Kariakoo imekufa, lakini Kariakoo imeuwawa na vitu viwili. Wataalamu wetu nafikiri hawajui kitu gani kinauzwa Kariakoo. Kariakoo haiuzi soda, haiuzi diesel, haiuzi vitu hivi ambavyo kwenye tarrif za TRA zinahesabiwa kwa tani na lita. Vitu vinavyouzwa Kariakoo ni vitu hivi vidogo vidogo. Nitatoa mfano uki-import glass Sheria ya TRA ina kitu kinaitwa tariff, tariff ya glass inaitwa glassware, lakini kuna glass ya shilingi 800 na kuna glass ya shilingi 10,000; TRA kwa kuwa anataka pesa atachukua glass ya shilingi 1,000 kwenda kui-charge 5,000 akikuwekea kwenye shilingi 5,000 hautauza na watu wote Watanzania, wa Malawi na wa Kongo wanafata hii glass ya shilingi 1,000 hawa watu wa Samora ndiyo wanafanya glasi ya shilingi 10,000. (Makofi)

Kwahiyo nafikiri TRA waangalie tariff ni kitu ambacho tuliki-download sisi kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyovunjika, ni vizuri TRA wachukue vitu waviainishe ili mtu alipie kwa kitu alicholeta, watu wote watarudi kama wenyewe watakubali watu walipie kwa kile kitu alicholeta.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi ukileta kontena moja la glass hutalilipia hapa, lazima ulipeleke Mutukula ukalipie Mutukula ili watu wachukue polepole na baskeli kuleta au ulipeleke mpaka Tunduma ili watu waanze kulileta kwa sababu watu wale kule Wazambia wanakubali ulipie kwa item uliyoleta, huku unatakiwa ulipie kwa tariff. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukileta nguo zinazouzwa Kariakoo ambazo ni t-shirt, t-shirt ziko za shilingi 3,000, iko t- shirt ya shilingi 20,000. Kwenye hesabu ya tariff unalipa excise duty, unalipa VAT halafu unaenda kwenye weight (kwenye uzito) na nguo nzito ni ile ya bei rahisi nguo nyepesi ndiyo ya bei ghali. Sasa haitawezekana ile nguo kuiuza ndiyo maana inakwenda nje halafu inarudi huku, nafikiri wataalamu wetu wa TRA... (Makofi)

MHE.SALIM HASSAN ABDULLAH TURKY: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Turky anayezungumza hapo ni Profesa sasa...

MHE. SALIM HASSAN ABDULLAH TURKY: Taarifa ninayompa maneno anayozungumza ni sahihi kabisa na ukienda kuangalia chupi ile ya kamba ndiyo ghali zaidi kuliko chupi nzima, ahsante sana. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kishimba unaipokea taarifa hiyo?

MHE.JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri wataalamu wetu wa TRA ni vizuri kabisa wakubaliane na wafanyabiashara, ni vizuri Mheshimiwa Waziri wa Fedha awaite wafanyabiashara wakiwa wametulia ili apate kabisa data ili turudishe soko letu la Kariakoo. Ni kweli kabisa wachangiaji wote wanaliongea hili na kwenye Kamati ya Bajeti tumejaribu sana kuliongea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa Benki Kuu ya Tanzania nafikiri wakati wowote itatangaza utaratibu mpya wa namna ya ku-import mali. Utaratibu uliopo unaotarajiwa ni kwamba mtu lazima atume pesa kwa TT kwenda kwenye source ya kununua.

Mheshimiwa Naibu Spika, tungeomba wataalamu wote kabla hawajafanya kitu labda na wao watoe watu wao waende kule Dubai na China waone mali inanunuliwa namna gani. Kule China na Dubai hakuna mahala unaweza kumtumia mtu hela ukazikuta hizo hela, watu wananunua kule wakiwa na hela cash kwa sababu hata mali aliyokuuzia anaweza akakuletea fake na ukirudi kwenye lile duka limekuwa saloon. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama utatuma hela toka hapa, utamtumia nani kule China au Dubai, haiwezekani, ndiyo maana tunaomba wataalam wetu basi labda wachanganye changanye na watu wa biashara kidogo ili wanachotengeneza kionekane cha Tanzania maana yake inaonekana kinachotengenezwa hata wananchi wanatucheka kwamba hivi hata ninyi Wabunge mnafanya nini huko maana yake kinachotoka ni kama kimetoka London. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo yote nashukuru naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimwa Spika, yeah, ahsante sana, naungana na Wabunge wenzangu kuchangia Wizara hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza nichukue nafasi hii kumpata pole Mheshimiwa Mbowe kwa ugonjwa wa mtoto wake huu wa corona ambao ulimpata. Nampongeza Mheshimiwa kwa busara kubwa sana aliyotumia kupambana na hili janga la corona, hasa kwa kuzingatia watu wetu ni matabaka mbalimbali, tuna wafugaji, tuna wakulima, tuna wavuvi, tuna wafanyabiashara, na tuna watu wa hali ya chini sana, Mheshimiwa Rais alichotumia kama asingetumia hekima leo nchi yetu ingekuwa na disaster kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano mdogo tu kwa sisi wafugaji au wakulima ukiambiwa kwamba usimtoe ng’ombe kwenda kuchunga ingekuwa kazi ngumu sana maana yake ng’ombe hata kama wewe mwenyewe umefariki ng’ombe lazima waende wakale. (Makofi/Kicheko)

Mheshimwa Spika, sisi tunalima mpunga…

SPIKA: Mheshimiwa Kishimba unavunja kanuni kumfikiria kwamba Spika amefariki. (Kicheko)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimwa Spika, hapana. (Kicheko)

SPIKA: Endelea kuchangia Mheshimiwa.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimwa Spika, tuna wakulima wa mpunga, wa mtama ambao lazima waende shambani kwenda kuangalia ndege ingawaje kama watu hawataruhiwa kutoka basi chakula chote kitakuwa sikukuu ya ndege. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri wote na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunaishukuru sana Serikali kwa kuondoa tozo la maiti kwenye hospitali wakati mtu amefariki akiwa anadaiwa, ingawaje baadhi ya hospitali bado wanakataa wakisema kwamba hawajapata waraka. Tunaomba Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya kwenye majumuisho yake ajaribu kutueleza vizuri au atoe waraka huo au atamke ili Sheria hiyo iweze kuanza kutumika hasa wakati huu mgumu sana wa watu wetu wanaokutana nao. (Makofi)

Mheshimwa Spika, tungeomba pia wenzetu wa hospitali na zahanati za binafsi wapunguze au hapa nusu mtu anapofariki, hali kule vijijini ni mbaya sana, sorry. Mwenendo wa ugonjwa huu wa corona ni hatari sana tungeomba Serikali kama inaweza kuwasamehe madaktari walioko Magerezani na Wauguzi wa afya ili waje tuungane nao watusaidie wakati huu. Vilevile kama inaweza Serikali madaktari na wauguzi waliostaafu kama inaweza kuwapa mkataba wa muda inaweza ikatusaidia sana maana yake wapiganaji wetu sasa hivi kwenye hii vita ni wauguzi wa afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba vilevile wenzetu wa Idara ya Afya kuna zahanati au hospitali ambazo wamezifungwa tungewaomba sana kama wanaweza muda huu wakarekebisha masharti ili hospitali hizo na zahanati ziendelee kuhudumia watu, itatusaidia sana maana yake hali ilivyo kama vile kama siyo watu wetu wa afya na Wizara ya Afya kufanya udhibiti ni vizuri watusaidia sana. (Makofi)

Mheshimwa Spika, napenda vile kuungana na wewe juzi hapa wakati wa mchango na Mheshimiwa mama Prof. Tibaijuka na Mheshimiwa Ngeleja waliliongea sana suala la dawa za kiejeji. Ni kweli tumekuwqa tukipambambana na mafua kwa muda mrefu sana na wenyeji wanaoutalaam wa mafua sitaki kusema kwamba ni corona, lakini ni vizuri wenzetu wa Wizara ya Afya wakafikiria sana suala la kuongea na wenyeji ili kupata mahala pa kuanzia tutegemea tu kwamba tunategemea kwamba lazima dawa ipatikane Ulaya, au chanjo ni kazi ngumu sana ni vizuri wataalam wetu waungane na wenyeji ambao wamekuwa wakipambana na mafua kwa muda mrefu sana kabla ya dawa za kizungu hazijaja, itatusaidia sana kupambana na hili tatizo najua wote tunakuwa na maeneo yanayoongewa mitaani ni kwamba inawezekana watu weusi wanaweza wakajidhibiti wenyewe au nini.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri wataalam wa afya wasiogope, na wasiogope kabisa kutamka kwamba kitu hiki kiko hivi kwa kuogopa kwamba labla watavunja wataalam wao, hapana ni vizuri watamke kabisa kwamba kitu hiki kinaweza kuwa hivi, kitu hiki kinaweza kuwa hivi, itatusaidia sana sasa hivi kuna mkakanganyiko mkubwa sana kila mtu anaamuka na la kwake matokeo yake watu wetu wanakuwa kwenye wakati mgumu sana ni vizuri watu wa Wizara ya Afya wawe na msimamo ambao utatuendesha vizuri kukumbana na hili tatizo.

Mheshimwa Spika, kuna hizi mashine za oxygen, tungeomba wataalum wetu wa afya watoe relief kidogo kama mtu anaweza kutengeneza hata kama ina capacity ndogo waruhusiwe kama za zamani zipo zifanyiwe marekebisho, kusema tu kabisa tunahitaji kupata kitu kipya, tunaona wenzetu wa Ulaya ambao wameendelea na ndiyo wanatengeneza wameshindwa kabisa machine hazitoshi, endapo tatizo hili litatokea tunaweza kuwa kwenye wakati mgumu sana. Tunaomba sana wenzetu wa afya Serikali iruhusu kama watu wanaweza kuagiza iwafikirie haraka ili hili tatizo tuweze kukabiliana nalo. Ni kweli kabisa Mheshimiwa Mbowe ameeleza vizuri kwamba suala hili ni bora tukajiandaa nalo hatuna namna yoyote ambayo tunaweza kukabiliana nalo maana yake liko kwa jirani zetu, vilevile linatuathiri kiuchumi.

Mheshimwa Spika, ni vizuri Mheshimiwa Waziri wa Afya akaitisha kongamano ambalo litajumuisha wataalam wote wa pharmacy watengeneza madawa, vilevile na waganga wa tiba za asili ili waweze kukaa pamoja tuweze kupata nini hasa kilichoko ndani ambacho kinaweza kutusaidia wakati tunasubiri dunia ifanye nini.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, amekuwa akifuatilia hoja zetu Bungeni, tulikuja hapa na hoja ya spirit ambayo ni gongo, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa amechukua gongo ile ameipelekwa kwenye maabara, na kwenye maabara imeonekana inafaa kuliko spirit zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunamuomba Mheshimiwa Waziri wa Afya sasa kwa kuwa wananchi wetu hawawezi kununua hizi sababu tunazotumia ambazo zina alcohol asilimia 65, atamke basi wananchi kwa muda huu wa dharura wanaweza kunawia gongo? Ili kuzuia hilo suala ya corona. (Kicheko/Makofi)

Mheshimwa Spika, hii sanitizer tunayonawia ina alcohol asilimia 65 na gongo ina alcohol asilimia 55, basi Mheshimiwa Waziri wa Afya kama anaweza kutoa sasa hivi msamaha huo ili iweze kutusaidia…

SPIKA: Jamani anayechangia ni Profesa naomba msikilize vizuri wengine hata hamjui alcohol content ya gongo. (Kicheko)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimwa Spika, nakwenda direct kwenye suala la uwekezaji maana yake najua Ofisi ya Waziri ndiyo inayohusika na uwekezaji, wote tumeuangalia kwenye eneo viwanda, mahoteli na maweneo mbalimbali. Lakini tunaomba Ofisi ya Uwekezaji iruhusu uwekezaji wa mawazo, mimi nafikiri ni uwekezaji mzuri kuliko uwekezaji wowote, nitatoa mfano ingawaje muda mdogo unakimbia. Nikiwa Zimbabwe ndiyo niligundua uchenjuaji wa dhahabu kwenye mchanga na kwa malundo ambayo yamekuwepo hapa ya dhahabu zaidi ya miaka 50 nilivyokujanayo hiyo teknoloji ilinichukua miezi miwili mitatu nikanyang’anywa, lakini kwa kuwa hakuna namna wala kitu unachoweza kudai sikuweza kufanya kitu chochote…(Makofi)

SPIKA: Ni kengele ya mwisho, nakupa dakika mbili umalizie.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimwa Spika, ningeomba Wizara ya Uwekezaji kama itatengeneza kitengo mtu akiwa na wazo kokote aliko ambalo akilileta hapa wananchi wanaruhusiwa kuli-copy, lakini yeye apate per cent kutoka kwenye lile wazo, maana yake wanachokamatilia wao ni wazo ambalo limeshikiliwa kwenye computer, lakini wazo ambalo ukilileta uwezi kuwazuia wananchi, lazima walichukue. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wenzetu wawekezaji wabadilishe mwelekeo ili tuelekee kwenye eneo lingine eneo la mawazo linaweza kuwa rahisi kuliko leo watu wanasema kwamba huyu kafa na dawa yake, lakini angesema huu mti ni dawa atapanda lini yeye, lakini wenyewe watasema ukitamka mtii huu ni dawa Mheshimiwa Dkt. Karemani ananitazama, wakisema hii ni dawa Mheshimiwa Dkt. Kalemani anayo dawa ya mifupa, kama anaweza kupewa ku-share kwenye kile kinachopatikana ingekuwa bora sana na tusingehangaika na mikutano na kitu chochote, mawazo dunia nzima inayo. (Makofi)

Mheshimwa Spika, kwa kumalizia bei ya dhahabu imeanguka sana, kwenye masoko yetu, lakini kwenye soko la dunia, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha anisikilize vizuri sana. Dhahabu imeanguka asilimia 50 mpaka 40 kwenye masoko yetu ya ndani, lakini kwenye soko la dunia haijaanguka, kwanini sasa Benki Kuu isiingie ndani ikanunua hiyo dhahabu kwa wakati huu ili iweze kupata hizo faida maana yake kuna gap kubwa sana kwenye siku kumi kabla ugonjwa haujaanza kudorora, lakini bahati nzuri kama wenyewe wanaogopa Benki Mkuu humu tuna Wabunge zaidi ya watano wanaoijua dhahabu vizuri sana, hata kama ni kuvunja kanuni basi awachukue hao hawa Wabunge waliomo humu ndani wasimamie zoezi hilo la ununuzi wa dhahabu ili Serikali ipate faida, ni vizuri sana wanasema kufa ni kufahana, ni vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Niungane na Wabunge wenzangu kwenye kuchangia Mpango huu wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo mawili au matatu kama muda utaniruhusu. La kwanza; juzi Mheshimiwa Rais alipita kule Kahama akiwa anatokea Chato, alisimama Kahama. Haikuwa nia yangu mimi kueleza matatizo yale ya shule na afya lakini ilibidi kuyaongea ingawaje ni mambo ya Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa shule wajaribu kuja na mawazo mapya. Hivi ninavyoongea Gazeti la Nipashe la leo wanafunzi waliochaguliwa kwenda kidato cha kwanza Mkoa wa Shinyanga ni 20,000 lakini wanafunzi 7,400 hawajulikani walipo na hawajahudhuria. Sijui sasa hata watakaokwenda form one, je watafika form four? Watakaofika labda robo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili wala siyo la Serikali kutoa pesa. Sheria ilizoweka na utapeli ulioingia shuleni, shule imehama kwenye elimu imekwenda kwenye biashara. Ukiiona orodha ya karatasi ya mwanafunzi kutoka darasa la saba kwenda form one, akikuletea mtoto utamwambia ngoja nile kwanza. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitu vinavyosemwa mle ndani mwananchi wa kawaida wa kijijini hawezi. Mfanyakazi wa kawaida wa mshahara wa laki tatu, hawezi. Vitu vinavyotakiwa ni kweli vitawezekana au tutaongeza rushwa? Wanakijiji wao wamekataa lakini mfanyakazi itabidi aende kwenye rushwa au aibe ili ampeleke mtoto wake shule.

MWENYEKITI: Unazungumzia joining instructions? Ile karatasi ya…

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, orodha ya vifaa vinavyotakiwa.

MWENYEKITI: Orodha ya vifaa ili aweze kujiunga na form one.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo. Orodha ya vifaa hivyo haina uhusiano wowote na elimu; ni utapeli mtupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanafunzi wa kijijini kweli anahitaji tracksuit; kweli? Mheshimiwa Waziri yuko hapa na bahati nzuri hizi ni ripoti za Shinyanga, tunaomba na Mheshimiwa Waziri, Uzuri Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango na Waziri wa Elimu wote ni wa Kigoma, watupe na wao ripoti zao kama kweli watu wa Kigoma wanaweza kununua viatu vyeusi. Kiatu cheusi original ni Sh.35,000 mpaka shilingi 40,000, hivi vingine vyote vinapigwa dye na Machinga vinakuwa vyeusi, baada ya wiki tatu vinarudia kuwa vyeupe. Sasa kuna sababu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Waheshimiwa hawa, Mheshimiwa Waziri wa Elimu ni Profesa, Mheshimiwa Dkt. Mpango pale ni doctor. Kweli na kutembea kote, leo bado tunahusudu viatu kweli viwe ndiyo chanzo cha elimu cha kwenda kumkabili mtu. Wenzetu wangeliangalia sana. Nusu ya wanafunzi hawakwenda; haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la elimu naona Wabunge wanajaribu kuliongeaongea lakini linahitaji maongezi marefu sana. Ni kweli mwanakijiji unamchukua mtoto wake asubuhi saa 12 unakwenda kumkimbiza mchaka mchaka baadaye anaingia darasani, saa tatu, saa nne. Kwa nini asiende saa tano amemsaidia mzazi wake asubuhi, amefanya na kazi ili aende saa tano amekula. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama tutakataa, tutafanyaje. Huko mwisho hatuna ajira, tunakuja kuwaambia warudi nyumbani baada ya kuwa na degree. Wewe ulimchukua mtoto wangu anakula mihogo na viazi, unanirudishia anakula chipsi, soseji na mayai unakuja kukaa naye vipi nyumbani. Haiwezekani. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Waheshimiwa mnacheka lakini ni ukweli kabisa, these are facts of life. Endelea Mheshimiwa Kishimba.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, unamrudisha mtu unamwambia akajitegemee, anajitegemea naye vipi? Sisi kule kijijini hata kuku akila mayai yake anachomwa mdomo na huyo ni yule anayetaga vizuri kama hatagi vizuri kesho yake anapelekwa kwenda kuuzwa. Sasa unanirudishia mtu anayekula mayai mimi nitakaa naye vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni vizuri wenzetu wa Wizara ya Elimu waje na mawazo mapya. Academy za mpira ninyi mnakubali watu wafundishwe wakiwa wadogo, mnakatazaje watoto wetu kulima, kuchunga asubuhi, kufanya biashara za duka ili waende mchana; kwani watapata hasara gani? Hata kama ikitokea akawa mtoro ameshajua biashara kuna ubaya gani? Mtuambie ubaya wake nini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ninyi wenyewe mna-confirm, Mheshimiwa wa Mipango kule amesema ana watu wana miaka nane hawana kazi, je, familia zao mnazihesabuje na ninyi Serikali mnataka hela yenu. Mimi nilikuja na hoja hapa kwamba na watoto wawe wanalipa. Lakini wewe unang’ang’ania mpaka riba kwa mtoto. Vipi mimi mzazi, umeniacha maskini, mtoto wangu umemharibu; hukumpa elimu, umemharibu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya Tanzania ukweli ni kwamba mimi natumia gharama kubwa kumwandaa mtumwa atakayeenda kuwa mtumwa wa mtu mwingine. Inawezekana kweli? Kwa nini unakataa mawazo yangu ya shughuli zangu tuka-share pamoja ili mtoto atakaposhindikana, akirudi kwangu mimi siyo mzigo, anajua hata vyakula vyangu na maisha yangu ya nyumbani; tungegombanaje na nani angekwambia kwamba kuna tatizo la ajira. Ilikuwa hakuna tatizo la ajira maana yake mtoto angeona kwamba kazi ya biashara, kazi ya kulima au kufuga inanilipa Zaidi, sitaki hata hiyo ajira, ata-bargain na mshahara. Sasa hivi hawana haja ya ku-bargain mshahara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimnaulishe mwanangu, kila kitu, halafu mimi unipe karatasi nije kwako. Kwa kweli ni kitu ambacho kina matatizo makubwa sana. Uzuri kwa kuwa na Wabunge wengine, miaka mitano mimi nimepiga kelele lakini uzuri na Wabunge wameanza kuliona na najua mpaka mwakani wakati hela imepungua ndiyo tutalijua vizuri zaidi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili la uwekezaji. Mtazamo uliopo tunatazama tu upande mmoja. Juzi kwenye Kamati yangu ya Biashara na Viwanda nilijaribu kuwadokeza kidogo wenzangu kwamba jamani hivi uwekezaji ninyi mnaoujua ni wa viwanda peke yake. Dunia imebadilika, leo ndege yetu inakwenda India asilimia 90 ya wasafiri ni wagonjwa, kuna ubaya gani wenzetu wa uwekezaji wakaongea na watu wa hospitali za India waone kitu gani kinachowakwaza kuja kuweka hospitali zao hapa. Tuwaruhusu, tuwape EPZ ileile ambayo tunaitoa kwenye viwanda, tusiwawekee tena yale masheria yetu ya hapa wenyewe wafanye bila kufuata sheria za kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itatusaidia na wagonjwa wa nchi zingine wanaokwenda India watakuja kwetu, lakini watumie sheria za kwao, tusiwawekee tena yale makorokoro yetu, mara migration, mara hukusoma, mara nini, hapana, itawezekana kabisa na biashara itawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengi sana, kuna maeneo ya vyuo vikuu vya nje, tuwape maeneo au tuwajengee. Kama tunaweza kujenga vitu vyote vikubwa, tuwaulize wanataka nini, ili tuwajengee waweke standards zao, wanafunzi watoe wao nje, wa kwetu nao wakitaka wa- apply kama wanaenda nje, lakini wakiwa hapa hapa nyumbani. Nasi tukitaka kutibiwa kama ni hospitali, badala ya kwenda India, si tuta-apply tunaenda kutibiwa mle mle tu; na watu wa nje watakuja. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri wenzetu wa Uwekezaji mawazo yabadilike sana. Leo kuna biashara kubwa sana ya imani. Tuna viongozi wa dini ambao wana mvuto mkubwa sana. Kwa nini tusitenge maeneo tukawauliza, je, tukikujengea eneo la kuabudia, unaweza kuja hapa kwetu mara moja kwa mwezi? Ili kusudi wale watu wanaokufuata wewe kule wa nchi za jirani wanaweza kuja kukuona hapa mara moja kwa mwezi. Sisi tutapata biashara, hoteli zetu zitapata wateja na maeneo yote ya shughuli mbalimbali yatafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilienda mbali sana mpaka nikasema, hata group lile la Babu wa Loliondo, kuna ubaya gani na wao wakawekewa eneo lao na yenyewe ikawa EPZ. Mtu akitaka kwenda kutazamiwa hali yake, aende kihalali. Si tumeruhusu? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachohitaji sasa hivi ni kutembelewa. Hotuba ya Mheshimiwa Rais imesema inataka watu milioni tano, je, watu milioni tano tutawapata kutokea wapi ili waje watutembelee? Ni lazima wenzetu wa Uwekezaji wapanue wigo, waache kufikiria upande mmoja. Wakijitahidi hilo, litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kumalizia ni suala hili la permit. Kuna shughuli ambazo huwa hazisomewi, ni za ukoo au mtu anaijua bila karatasi. Mheshimiwa Waziri wa Madini anafahamu, kulikuwa na suala la wakata Tanzanite. Wale watu wanaokata Tanzanite hawana elimu wala cheti, lakini wanafahamu kukata Tanzanite. Swali lililokuwa linatatiza, hawawezi kuja hapa kwa sababu permit yao haiwezi kupatikana maana hawana elimu. Sasa labda niulize wasomi kwa kuwa wamo humu; definition ya elimu ni nini, ni karatasi au ni kuelewa? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana kama mtu umemkuta anakata Tanzanite vizuri na anauza; na yako inakwenda kukatiwa hapo, unashindwa kumwambia aje huku kwa sababu ukimwuliza cheti, anasema sisi hii kazi haisomewi na vyuo vyake havipo. Sasa kweli tukose biashara kwa ajili ya neno “cheti” au “document” na mtu anafahamu? Haiwezekani! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango ni mzuri, naomba sana wenzetu wa Uwekezaji na Mheshimiwa Waziri wa Fedha wafikirie.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu ya juu, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Waziri wa TAMISEMI kwa zoezi waliloanza sasa hivi la kupeleka wanafunzi kwenye vyuo vya VETA kwa muda wa miezi sita ninampongeza sana. Ninaona suala langu kidogo umelianza lakini lipo eneo lile lile, juzi hapa kulikuwa na mjadala kati ya Mheshimiwa Nyongo na Mheshimiwa Waziri, kuhusu suala la watu stress sijui presha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Waziri miongoni mwa asilimia 50 ya presha ambayo wazee na watu wanayo sasa hivi ni suala la elimu, na suala hili la elimu sio kwenye elimu yenyewe kama ulivyosema. Leo bahati nzuri ulivyosema nimekuja na sample hapa nina sample ya daftari ambazo zinasomea shule za private, shule ya private inasomea daftari la shilingi 200 ambapo kwa mwanafunzi kwa madaftari 11 itakuwa shilingi 2,200 lakini shule ya Serikali inasomea counter book. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, counter book 11 ni sawa sawa na shilingi 55,000 kwa kijijini ambao ni sawa sawa na gunia zima la mpunga au mahindi. Sasa inawezekanaje matajiri wakasomea daftari la shilingi 200 maskini wakasomea daftari la shilingi 5,500? Na mnasema kwamba watu wana stress ni kweli watu hawana raha na shule, hawana raha wananchi na shule nina-sample ya uniform hapa. (Kicheko/Makofi)

(Hapa Mhe. Jumanne K. Kishimba alionesha mfano wa uniform)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, uniform za private ni rangi hizi (blue bahari) uniform za shule za Serikali ni rangi nyeupe ni vipi mzazi ataweza kufua kila siku, haiwezekani Mheshimiwa Waziri wa Elimu na TAMISEMI wote ni Wabunge wa kuchaguliwa ni kweli ni sahihi? Kwanini private wasomee za rangi wanafunzi wa shule za Serikali wasomee nyeupe. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo kutwa nzima wazazi wanaendelea kushinda wananunua sabuni na kufua, tunaongeza umaskini badala ya kuongeza elimu. Ni kweli Mheshimiwa Waziri ni lazima kabisa alifikirie upya wananchi wamechoka hawataki kabisa shule, kwasababu sasa hivi kijijini ukifika unakuta mahali unauliza ng’ombe za hapa mlizipeleka wapi? wanasema ng’ombe amemaliza ndugu yako shuleni, hakuzimaliza kwa ajili ya kulipia shule alimaliza kwa ajili ya kulipia vifaa vya shule ambavyo havihusiani na elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matokeo yake mtu anaona bora kuzaa watoto wajinga huwezi kufilisika kuzaa kuliko kuzaa watoto wenye akili. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunamuomba sana Mheshimiwa Waziri na Waziri wa TAMISEMI walifikirie sana. Nakuona kila siku unalalamika kwamba timu zetu za Taifa watu hawana nguvu lakini watoto wanatoka asubuhi wamebeba huo mzigo uliousema sasa hivi wa hizi counter book 11 wana miaka minane mpaka saa tisa jioni wamekataliwa kubeba chakula kwamba kinaitwa kiporo. Kilibatizwa kitaitwa kiporo wanakwenda bila kula, lakini je wakirudi kutoka shuleni kuna mzazi atapika chakua fresh kwa yule mtoto, si atampa kiporo, sasa ulimkataliaje kubeba kiporo asubuhi kwenda nacho shule. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, matokeo yake sasa hivi unaweza ukaongea lugha nyingine ambayo sio nzuri, lakini watoto hawana afya, hawali chakula. Sisi Waislamu tumefunga lakini tunakula daku saa kumi lakini saa saba ukikutana na Muislamu mkali kama pilipili na ni saa saba mchana. Vipi huyu mtoto wa shule ambaye alitoka saa 12 hajala kitu chochote kule kwetu vijijini hakuna chai wewe mwenyewe unatoka huko. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hakuna chai anakwenda mpaka kule anarudi saa tisa, saa tisa kama walikuja wageni walipewa kile chakula wakakila anaambiwa subiri usiku atakuwa na afya huyo mtoto? Na hizo mimba mnazosema za shuleni zitakosekana kama mtu ameshinda bila kula ataacha kutongozwa kweli? Ni kweli twendeni kwenye mambo ambayo yapo straight kabisa. Wenzetu Wizara ya Elimu lazima wafikirie haiwezekani leo hii kwenye shule za University wame-introduce tena wanataka simu ya WhatsApp wanataka na laptop.

Mheshimiwa Spika, ukiongea laptop kwa mtu wa kijijini au mama ntilie na simu ya WhatsApp ni shilingi Milioni 1,000,000 tayari kuna miji haijawahi kuishika laki 500,000 kwa miaka 30 anaweza akafanyaje huyo mtu? Lakini je kweli toka mme -introduce hizi laptop na hizi elimu imepanda? Na je, watu wamekuwa efficient? Kwa kuwa leo mmeweka laptop mbona ndio mdololo umeongezeka zaidi. Haiwezekani lazima wenzetu wafikirie upya, wanawabebesha mizigo mizito mno wazazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunalazimishwa vitatu unaambiwa kiatu cheusi kweli inawapa wazazi wakati mgumu mno kila unapofika kijijini ukiwaita watu kwenye mkutano kuwaambia habari ya shule baada ya dakika 10 unabaki una watu sita tu. Maana yake wanaona umewaletea lile zimwi ambalo linakula haliishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naungana sana na Mheshimiwa Mpima maneno aliongea mengi kule kuhusu suala zima la elimu ni kweli kabisa kunahitaji mabadiliko makubwa. Lakini kabla ya mabadiliko Mheshimiwa Waziri atupe waraka unaoonesha kwamba wanafunzi wanatakiwa wasomee nini.

Mheshimiwa Spika, wa tajiri aje la laptop wa maskini atengenezewe hata internet cafe pale shuleni ili walipe shilingi 500 waangalie hizo laptop mnazotaka wa download watoke lakini sio kuwabebesha laptop.

Mheshimiwa Spika, leo hii wote humu ndani ni wazazi kila asubuhi unagongewa hodi na mtoto na ndio wanamwambia mgongee wewe hawezi kukasirika, ukiamka asubuhi unawakuta wanne wanataka hela ya kwendea shule wakanunue chakula kweli itawezekana na kila siku utalala na chenji? Je hatuoni kama watoto tunawafundisha wizi maana yake kila wakirudi ukiwauliza chenji wanasema tulinunua hiki, tulinunua hiki wana ku- blackmail je, huyu mtu baada ya miaka 10 hatakuwa mwizi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si atakuwa mwizi sasa mnakataaje watoto wasipike chakula wao wenyewe asubuhi waondoke nacho waendenacho shule, na vile vile kama tunawakatalia wakale maandazi na mikate! Je, maandazi na mikate yenyewe sio kiporo, si mkate una-expire baada ya siku 14 sasa haujawa kiporo na una amira. Kwa hiyo, tunamuomba Waziri wa Elimu wafikirie kama tunawatumikia wananchi wa Tanzania ambao ni maskini, hapa hatuna mpango wa kumjadili tajiri, tajiri atapeleka private atapeleka kila mahali private lakini sisi tunayemjadili ni mtu maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni suala hili ya University ni kweli ukiongea wakati mwingine unaweza kuwa kama unaongea kichwa kama hakipo. Lakini makampuni yote duniani sasa hivi yanafanya biashara yanakwenda yanatafuta wateja yanatafuta hiki, lakini sijaona University wakiwatembelea watu waajiri haijatokea kwa wale watu wa University ni kwasababu wao wanasukumiwa wateja kwa hofu ya dunia kwamba usiposoma shauri yako. Kwa nini na wao wasiwe wanaenda wanatatufa kazi kwenye makampuni ndiyo wanatangaza kwamba bwana sasa hivi tumepata kazi NBC mshahara shilingi 800,000, tumepata NSSF na Bakhresa, kwa hiyo, tayari tunazo nafasi za kazi 4,000, kama unataka kusajili lete shilingi 10,000,000 baada ya kupata degree na kazi hii hapa.

Mheshimiwa Spika, nalisema kwa mara ya kwanza duniani linaonekana kama ni neno la kipuuzi, lakini inaweza ikasaidia sana kwa sababu inawezekana hata ile elimu wanayotoa wao, wale watu wa ajira hawaihitaji. Kama watakuwa wameongea na mwajiri atakuja sasa kuuliza nataka niwaone vijana wangu kama wameelewa. Inawezekana muda wa kusoma badala ya miaka mitatu ya degree ya biashara ikatosha miezi minane huyu benki akasema mimi wananitosha nipe nikaanze nao. Kuliko sasa hivi mimi nikishasema ni Profesa nina degree kazi yangu inakuwa ni kuchukua milioni 10 za watu na kuwa-dump, haiwezekani ni lazima na vyuo navyo viwe committed pia, vikatafute na vyenyewe ajira ndiyo visajili. Vyuo vikaongee na waajiri ili hata hiyo mitaala vitaibadilisha sasa kulingana na soko lenyewe watakalokutana nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala hili la elimu kwa kuwa Mheshimiwa Rais ameliongea vizuri tuanze kulijadili kwa mapana. Mheshimiwa Mpina na Mheshimiwa Sima wameliongea lakini kwa nini elimu tunaiongea Kizungu peke yake, kuna ubaya gani watu wakafundishwa kuchunga ng’ombe za kienyeji shuleni ni kosa? Mwalimu mle ndani akawemo Mmasai, Msukuma au Mtaturu akawa anawaambia ili ufuge ng’ombe wa kienyeji unatakiwa uwatoe asubuhi kwa mwelekeo huu, uwapeleke maji kwa mwelekeo huu, je, itakuwa ni kosa? Ni lazima mtu afundishwe Kizungu? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, maana karibu wanafunzi wote wanarudi kijiji sasa hatuna mwalimu, kama alivyosema Mheshimiwa Mpina elimu ya biashara inafundishwa na Profesa wa biashara lakini hajawahi kufanya biashara. Kwa nini hatuna kitabu cha Bakhresa au Mohamed Enterprise ili tukitumia kwenye masomo tukafanye biashara? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kama tumesema elimu iwe wazi tusiifichefiche kama uchawi tuendee nayo tu moja kwa moja. Madaktari wanasomea hospitali ndiyo maana hatuna mgogoro na daktari lakini huku kwingine unasomea manunuzi, mnaita procurement kweli manunuzi ni miaka mitatu, unajifunza kununua nini miaka mitatu. Haiwezekani manunuzi miaka mitatu kweli inawezekana? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, wale wazazi kule mtoto hawamuoni, unamrudisha kule ni miaka 25 ukimuuliza umesomea nini, anasema nimesomea manunuzi. Sasa haya maduka yote nani atakuajiri maana watu wote wananunua bidhaa zao wao wenyewe. Haiwezekani! Tuongee moja kwa moja ili wananchi waanze kuona kweli tunaongea kitu ambacho wanakielewa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango huo kwa kumalizia tu, nimuombea Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI watupe regulation ya mahitaji ya shule ili na sisi iwe rahisi kuwajibu kule majimboni kwetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hivyo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nakupongeza wewe, Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichonipelekea kuchangia kwenye Wizara hii ni kitu kimoja tu. Kuna sheria mpya hapa ame-introduce Mheshimiwa Waziri, ambayo inamtaka mtu atakayekuwa na gunia moja la mkaa, ni lazima akapate kibali kutoka Halmashauri ya Wilaya na awe na EFD machine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda wenzetu wangejaribu kuangalia jiografia ya nchi, maisha ya wananchi wetu yalivyo unapotaka kutengeneza kitu kama hiki. Ina maana tutarajie ndani ya mwezi mmoja kutatokea chaos kubwa mno ya mkaa. Je, itawezekana? Yaani kwa kawaida itawezekana watu wasipike kweli na wasile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Wizarani labda wawe wanajaribu kuangalia yanayotutesa kule majimboni. Kuna majimbo mengine kutoka kwenye Makao Makuu ya Halmashauri kwenda kule kijijini ni zaidi ya kilomita 200. Mwananchi anataka gunia moja la mkaa kwenye mti wake mwenyewe, kweli aende mpaka wilayani apate na EFD machine! Anaipata wapi EFD machine mtu wa gunia moja? Ni kitu ambacho wala hakiwezekani wala hakiingii akilini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii vita ya mkaa na kuni toka tunapata uhuru, toka wametuachia Wakoloni: Je, watu milioni 60 wanaotumia mkaa na kuni itatokea wataacha kula? Nani ataibuka mshindi kwenye hii vita? Kwa nini Wizara isirasimishe hii biashara kama tulivyofanya kwenye madini? Dhahabu tulihangaika miaka 50, lakini ilivyorasimishwa, leo hatuna matatizo na biashara ya madini. Kwa nini mkaa na kuni usirasimishwe ukaenda halali, wao wakachukua ushuru wao kwenye gulio, wakapanga kabisa pale kwamba hii miti ya Serikali ikae hapa/mbao za Serikali zikae hapa, mkaa wa Serikali ukae hapa; mkaa wa mkulima mwenyewe mti ukae hapa ili biashara hii iwe halali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu, yeye TFS au yeye Wizara ya Maliasili na Utalii, anao kweli askari wa kutosha kuwazuia watu milioni 60 wa Tanzania wasipike? Yeye mwenyewe hapa amekula chakula cha mkaa, sisi tumekula chakula cha mkaa, anayekamata amekula chakula cha mkaa. Itawezekana? Ni kitu ambacho hakiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sababu ya kupigana vita usioshinda? Leo mkaa, kwa wenzetu Namibia na South Africa inaitwa dhahabu nyeusi, ni fedha. Sasa kama leo unasema kwamba huyu mwananchi tukamzuie kuchoma mkaa, nawe unatuambia tukamwambie apande mti, anapanda mti kwa ajili ya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake, sisi kwetu huko Kanda ya Ziwa ukimwambia mtu apande mti kwa ajili ya mvua, anakuona wewe ni mpuuzi. Maana tuna mafuriko miaka miwili. Atakuuliza: Je, unataka tupande miti ya kuzuia mvua? Maana yake ukiwaambia unataka miti ya mvua, wanakuuliza kuzidi hii iliyopo leo? Hii mvua iliyopo leo unataka izidi hapa? Ilitakiwa sisi tukawaambie panda miti ya kutengeneza fedha, ndiyo wananchi watapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine mnasema labda tunawasakama wasomi, lakini jaribuni kufikiria maisha halali ya wananchi. Jiji la Dar es Salaam au Mji wangu wa Kahama, ukiuzuia mkaa kwa siku nne, unategemea nini? Maana yake yule mchoma mkaa hana ulazima wowote, ni mtu yuko porini, ataacha kuja kuchukua kibali. Sasa vipi hawa watu wa mjini, unataka gunia la mkaa lifike shilingi 300,000/=? Unao mkaa wewe wa ku-supply? Ni kitu ambacho lazima wenzetu wafikirie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Tanzania ni nchi ya nne kwa ku-export mkaa wa magendo na TFS hajawahi kutoa export permit ya mkaa, lakini kwenye data za World Bank inaonyesha ni ya nne. Sasa unakataaje kurasimisha ili upate hizo fedha na wale wanaonunua wa magendo waje wanunue pale kwenye soko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri wenzetu wataalam lazima wafikirie sana. Haiwezekani baada ya miaka 60, kweli watoto wasome waende wakawe mgambo wa kukamata wazazi wao, ni sawa kweli! Haiwezekani! Kazi ya elimu duniani ni kutatua matatizo. Leo, Wazungu wametengeneza mpaka mapapai ya miezi sita. Wazungu wametengeneza kuku wa kizungu baada ya kuona kuna tatizo la kuku wa kienyeji na mayai yapo ya kizungu. Kwa nini hawa wataalam wasipande miti, wasilete miti ya miezi sita ili watu wakawa wanapanda miti wanauza kuni na mkaa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kurudi kwenye eneo la ugomvi, ugomvi, ugomvi, haiwezekani. Lazima twende kwenye pesa. Ina maana sasa hivi wao wanaenda kuanza fine, utawafunga watu milioni 60! Halafu mnataka hao watu tukawaombe kura. Unaweza? Unaweza ukaomba kura kwa watu uliowakatalia kula? (Makofi)

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Karibu.

T A A R I F A

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba kesi zote zinazohusisha misitu ni kesi za uhujumu uchumi. Sasa na mkaa utaingia huko: Je, nchi hii itakuwa na nusura? (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kishimba, unapokea taarifa?

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono mitatu. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Haya, endelea.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, najua na wewe ni graduate. Tunataka wasomi mtuletee mabadiliko. hatutaki wasomi kuwa Polisi, tunakuwa na majeshi mangapi? Tuna Jeshi la Polisi, tuna Jeshi la Wananchi, tutakuwa na majeshi kutwa nzima, haiwezekani. Tunataka mkaa ugeuzwe kama alivyofanya Mheshimiwa Dotto kwenye dhahabu. Sisi tumekaa gerezani miaka 20 kwa ajili ya dhahabu, lakini leo dhahabu si imekuwa halali? Ambayo ni sahihi. Kweli twende kuwaambia wazazi wetu kwamba tunakuja kukamatwa shauri ya miti. Sasa wanafanya nini? Haiwezekani tupeleke uhujumu wazazi wetu kwa ajili ya miti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana wenzetu wa maliasili, wajaribu kuangalia kabisa maisha ya watu. Tunapoongea, leo Jiji la Dar es Salaam ukiangalia matumizi ya mkaa ni makubwa mno. Kwa nini kusiwe na soko tu kesi hii ikaisha, wakachukua na ushuru wao pale pale; ili iwe ni kitu huru na kila mtu apende kupanda mti? Kupanda mti ni rahisi zaidi kuliko kulima mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri ajaribu kutoka kwenye Sheria za TFF. Maana yake TFF najua ndiyo yenye sheria ngumu sana, naye najua alikuwa kiongozi wa TFF. Ni kweli! Alikuwa TFF kwenye mpira, nafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba sana wenzetu, kuna suala hili la mifugo. Kwa kuwa wewe mwenyewe ni Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Viwanda,
Mazingira na Biashara…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Ni kengele ya pili?

MBUNGE FULANI: Ya kwanza.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wewe ndio Mwenyekiti wa Kamati yetu, najua hiki tunachoambiwa kwamba ng’ombe kwenye mapori yale ambayo hayana Wanyama, kwamba ng’ombe wanaharibu mazingira; unaonaje tukiteuliwa Wabunge watano na wataalamu watano, tuchukue ng’ombe 100 tukakae mle porini siku nne tuchunge wale ng’ombe, tuone physically uharibifu unaosemwa? (Makofi/Kicheko)

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Karibu Mheshimiwa, Doctor.

T A A R I F A

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nimpe mzungumzaji taarifa kwamba kuna model za ufugaji wa mseto kati ya wanyamapori na mifugo ambayo imeshafanywa hapa Tanzania na hata Kenya. Tanzania kuna Ranchi inaitwa Manyara Ranch Mkoa wa Arusha, kuna mifugo maelfu pale na wanyamapori; ni njia ya wanyamapori na hatujaona madhara. Kule Kenya kuna Ranchi inaitwa Ol Pejeta ina hekta 95,000, kuna mifugo zaidi ya 5,000 na wanyama wa kila aina, hata faru weupe wapo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Unapokea hiyo taarifa Mheshimiwa Kishimba?

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina nia ya kupingana na elimu, lakini hao walimu wenu wanaowafundisha, waliwahi kuchukua ng’ombe 100 wakakaa porini ndiyo wakaandika huo uharibifu? Maana yake tunashinda tunazozana tu na wananchi mpaka wananchi wanaona kama hata na nyie Wabunge ni wapuuuzi tu. Hivi kweli, ng’ombe anafanyaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna wanyama mle porini. Sawa, wananchi wako tayari kulipa, lakini watu wa maliasili wanachukua hela, wanaweka ng’ombe. Kwa nini tusiende nao tukaka humo siku tano tuone physically kwamba hasa huwa kinaharibika nini? Maana tukikalia tu makaratasi na kusomewa risala, uharibifu wa mazingira; itakuja kuwa mpaka lini? Wenzetu wanatengeneza pesa, hatuwezi kukaa na mawazo ya makaratasi kwa sababu tu mtu mmoja amesema, yeye amesoma; uharibifu wa mazingira alisomea London. Sasa wewe, tunataka kama ulisome London, utuletee mawazo ya kupata pesa, hatutaki mawazo ya London kuja kutukwamisha sisi, hapana. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine huwa sipendi lugha ya Musukuma, lakini kuna wakati kwenye hili, inabidi niungane na Mheshimiwa Musukuma. Kweli inauma sana. Anakuja kijana kasoma, anasema hamruhusiwi kupikia mkaa, hamruhusiwi kuni, ni uharibifu wa mazingira. Kuni sisi tunachukua matawi. Leo ukitembea na gari usiku au mchana, wazee wamebeba matawi, hakuna mtu anakata gogo la mti. Sasa unawakatazaje? Hao unaowakataza, ndio walikusomesha wewe na ndiyo wanaolipa kodi. Hiyo degree yako unaongea kiingereza, si ndio hao wanaotoa hela? Sasa unawakatazaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitegemea wewe umesoma, uje ulete mawazo kama Wazungu wanavyofanya. Mimi nimetoka Ulaya, nimekuja na miti ya kisasa, inaota miezi mitatu, unakata mkaa, unauza kwa pesa. Tunataka hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, nashukuru sana, lakini namwomba sana Mheshimiwa Waziri…

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi naungana na Wabunge wenzangu kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri wa Elimu na timu yake nzima kwenye marekebisho makubwa aliyofanya kwenye mitaala ya elimu kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wetu mkubwa ilikuwa ni mtaala mzima wa elimu ambao ulikuwa unaleta shida sana, kwamba mtoto aliyesoma ndiyo anakuwa mgogoro zaidi na taabu ngumu zaidi kwa mzazi kuliko yule ambaye hajasoma. Mzazi anateseka, Serikali inateseka na mpaka mwisho hatupati ufumbuzi, lakini kwa mtaala huu alioleta Mheshimiwa Waziri kama hawakuuchakachua wenzetu wasomi, unaweza ukatusaidia kutufikisha mahali pazuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana sana na Mheshimiwa Shigongo alivyosema. Ni kweli kabisa elimu ya sasa hivi Mheshimiwa Waziri, ilikuwa kama gereza, hauna uhuru nayo wewe mzazi. Sasa hivi kwa mtaala huu tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri katutofautishie sisi wa vijijini na wale wa mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijijini Mheshimiwa Waziri, watoto wetu sisi ni rasilimali ya kuzalisha mali ndiyo baadaye anaanza shule. Ninyi huku mjini Watoto wenu ni watoto wenye gharama. Kwa hiyo, lazima tutofautishane hapo. Sisi wa kwetu akiwa na miaka minne anaanza shughuli za kilimo pale nyumbani na kuchunga mbuzi, anang’oa mbegu za mpunga anakusaidia kupanda. Kwa hiyo, msije tena mkaleta hapo mkasema, aah sisi mambo human rights, watoto wanateseka, Hapana! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hawa watoto ndiyo wanaolima huu mchele mnaolia kila siku kwamba umepanda bei. Nani mzee anayeweza kuinama kutwa nzima kwenye tope kama siyo watoto? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tunaomba sana kwa kuwa umefungua kwamba mzazi akiwa na shida kesho kwamba ana shida, ana kazi yake nyumbani aje aombe ruhusa shuleni kwamba naomba mwanangu, siku tatu tukafanye naye kazi ili baadaye atakuja shuleni Jumatatu. Itatusaidia sana kwa ukubwa huu ambao umeufungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile elimu hii lazima iwe wazi na iwe nyepesi hasa darasa la kwanza. Afundishwe mtoto kitu chenye faida maana yake unaponiambia mimi nikajitegemee lazima kiwepo kitu kinachonivutia, kwamba unaniambia mimi nilime mahindi lazima unieleze kwamba punje fulani, miche fulani ukimwagilia ndoo moja ya gharama hii utapata shilingi hii, ili huyu mtoto awe na interest ya kwenda kufanya ile kazi akiwa bado mdogo. Itatusaidia tumepiga kelele sana muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata mimi nikifika darasa la nne Mheshimiwa Waziri nikawa mtoro lakini ukanifuata ukanikuta kwenye mahindi nalima mahindi ni kosa? Litakuwa kosa gani? Niruhusu nisome hata jioni kama unaona nashinda kwenye mahindi, nisome jioni nitalipa hiyo gharama kwa sababu hii siyo dini, hata dini ina option, kwamba kama hukusali Saa Saba au hukusali Jumapili sala ya asubuhi unaweza kusali ya Saa Saba ili kusudi maisha yaweze kwenda wakati mtoto anasoma na mzazi yuko na mtoto wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la VETA. VETA Mheshimiwa Waziri waongezee mitaala. Tunapoongea hapa VETA hana mtaala wa simu, hana mtaala hata wa television, hana mtaala wa pikipiki. Leo kuna market kubwa sana ya wafanyakazi wa ndani, VETA hana mtaala wa wafanyakazi wa ndani. Utajiri wa nchi za Asia ni wafanyakazi wa ndani. Ninyi mnasema mnafundisha hotel management, kutenga ugali unahitaji kusoma? Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfanyakazi wa ndani leo hii wote ni mashahidi ukitafuta mfanyakazi wa ndani unampigia Mheshimiwa Jesca kule Iringa unamwambia nitafutie kijana kule mlimani utafikiri unatafuta mbuzi wa mizimu. Yaani ni kazi kweli ni soko kubwa sana. Tulikuwa wote pamoja kwenye mtaala wa elimu, yule jamaa kutoka Philipines alivyosema kwamba utajiri wa Philipines ni wafanyakazi wa ndani ambao wanakwenda nchi za nje. Tunakuomba Mheshimiwa Waziri wa Elimu weka wafanyakazi wa ndani kwenye mitaala yetu itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakwenda kwenye suala moja ambalo najua ni gumu sana. Tumeruhusu msichana akipata mimba aendelee na shule lakini wanaopata mimba wanaweza kuwa wamebakwa labda mbili, asilimia 98 walielewana lakini sheria yetu inasema na huyu atatumikia kifungo cha miaka 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu yetu ambayo mliitoa mwaka jana Wizara ya Elimu, waliopata mimba shule ya msingi walikuwa 3,850, sekondari walikuwa elfu nane na kitu na ninafahamu kabisa hiyo takwimu kwa sababu kuna maelewano mengi sana kule kijijini, inawezekana msingi walikuwa zaidi ya 10,000, sekondari walikuwa zaidi ya 20,000. Sasa Mheshimiwa Waziri ina maana hawa 40,000 watapatikana watoto 40,000, baba zao watakuwa gerezani. Mwakani tena watapata mimba wengine 80,000 lakini tutakuwa na wafungwa tena 80,000. Je, magereza yetu inaweza kuwabeba? Je, hawa watoto watakapokua wakute wazazi wao wako gerezani miaka 30 watamlaumu nani na kosa lao kubwa nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni swali gumu, ni kazi yetu Wabunge maana yake tunaamka asubuhi ukiamka nyumbani watu watatu unakuta wana mtoto, kwamba baba yake alifungwa au alitoroka na mimi mtoto wa shule nimeruhusiwa kwenda shule lakini na nyanyaswa pale nyumbani. Mnafahamu wote makabila yetu au wenzetu mnatoka Uingereza? Makabila yetu mnayafahamu msichana anapozalia nyumbani hapendwi na kaka kwa sababu kaka alitarajia kupata ng’ombe 40 nae aoe, mzee naye alitarajia kukaa high table, naye hampendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huyu msichana anabaki na mateso, na mume naye ametoroka. Sasa Mheshimiwa Waziri labda tulilete kisheria tuone wale ambao hawakubakwa, huyu mwanaume aozeshwe huyu mtoto, aozeshwe huyu msichana ili huyu msichana aendelee na shule akiwa ameolewa. Maana yake hii shule ni kambi tu wazungu walituletea? Shule ni kambi tu siyo wala kitu chochote. Sisi Waafrika hatukuwa na shule. Hii ni kambi tumeletewa ikatengenezwa vizuri ndiyo ikawa shule. Sasa kweli watu wapoteze maisha yao baada ya miaka mitano tutakuwa na watoto laki tano hawana baba ila tuna wafungwa laki tano, magereza yetu yatatosha ukiunganisha na wafungwa wengine? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri sisi ambao tunaya-face hayo matatizo kule kijijini, maana yake mwenye mtoto wa kiume anakuja kukulilia kwamba mwanangu amepata matatizo amefungwa ana kesi. Mtoto wa kike naye anakuja pia anasema nina watoto wawili kweli nimeruhusiwa kwenda shule lakini hawa watoto sina wa kuwatunza, atawatunza nani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni swali gumu ambalo ni lazima Waheshimiwa Wabunge tulifikirie kwa mapana sana. Mimi sikatai sheria ya kwenda shule nakubaliana nayo asilimia 100, kwamba huyu aliyejifungua aendelee na shule lakini huyu mwanaume anaenda wapi sasa? Anaenda gerezani miaka 30. Mheshimiwa Waziri hiki ni kitu ambacho kiko nje ya utaratibu lakini ni dunia tunayokutana nayo, tutafanya namna gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, familia zingine wamekwenda watu mpaka wanne wapo gerezani lakini hawa wananchi wanakubali hawa waoane na huyu aendelee na shule. Nafikiri tulifikirie kwa mapana sana ili iweze kutunusuru kwenye hili tatizo. Tunaweza kuliona leo ni janga dogo lakini sisi kule vijijini ukiamka asubuhi ni mgogoro kweli. Unashinda kutwa nzima unampigia huku, unaenda gerezani kumuangalia huyu, unamsaidia huyu, mtoto hana baba na kote unakuwa unaendelea na mgogoro, kwa hiyo nashukuru sana Mheshimiwa Waziri kama utaweza kulifikiria kwa mapana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa Mheshimiwa Waziri niliwahi kuleta hoja hapa kwamba watoto iwe lazima kuwatunza wazazi siyo wajibu, lakini naona sheria hiyo bado. Mheshimiwa Waziri lazima tuifikirie kwa mapana sana. Mimi nimefanya kazi kubwa na mtoto wangu kutoka akiwa nursery school mpaka form six. Wewe Serikali umempenda umemuona ana akili umekuja kumchukua, anakuja kukufanyia kazi wewe, unamkopesha wewe na shule anasoma ya kwako, wewe faida unachukua wewe na anakuja kukufanyia kazi na unamkata. Mimi huyu mzazi wala hunisaidii, yaani hakuna chochote chenye value kwangu wala huna habari. Ni kweli mbona timu za mpira, mtu anapojua mpira anapocheza mpira si unapata na wewe uliyemtunza au timu iliyomtunza? Itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri na ninarudisha pongezi nyingi kwako na shukrani nyingi sana zimuendee Mheshimiwa Rais kwa kuturuhusu kulijadili hili suala la elimu na hadi tulipofikia sasa hivi nashukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. KIBERA J. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri pole sana kwa misukosuko unayopitia. Uchumi ni soko gumu sana hasa uchumi wa dunia ya tatu na nchi maskini kama Tanzania na hasa kuwatoa kwenye maisha waliyozoea kwa miaka 25 ni kama kumwachisha mtoto ziwa, lazima kuwe na mgogoro mkubwa, vuta subira!
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu, kwanza ni maoni kuhusu Serikali kuruhusu madini yetu na ya nje ambayo yanazalishwa na wachimbaji wadogo yawe asilimia zero wakati wa kuingia, kutoka iwe asilimia moja, itatusaidia sana kama nilivyochangia kwenye mchango wa bajeti mwezi wa Saba ulio kwenye Hansard ya Bunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara wa Kariakoo ni wachangiaji wazuri wa uchumi kwenye importation, lakini tatizo lao kubwa liko kwenye vitu viwili: Suala la TBS kwa product ambazo siyo chakula. Mfano, Redio ya sh. 5,000 wanataka iwe na ubora, lakini wananchi wananunua na wanasikiliza habari au muziki; wanawasumbua na ukizingatia mali nyingi inanunuliwa na watu wa Malawi, Mozambique, Zambia, Congo na majirani wengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tariff kwa bidhaa kwa mfano, Colgate gram 100 inauzwa sh. 2,000, Colgate herbal 100 inauzwa sh. 8,000. Kwenye tariff zinaitwa (Toothpaste) TRA anavyothamini ni sh. 8,000, muagizaji kaagiza kwa sh. 2,000, hapo ndipo mzozo unazuka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kufikiria upya suala la license kwenda kwenye mafuta ili kukusanya fedha kwenye ma- grader, tractor, generator na mashine nyingi, zitapunguza pia rushwa za barabarani.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, nampongeza Waziri, Naibu Waziri na Wabunge wote waliochangia Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda nitaongelea suala la upungufu wa chakula kwa baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na Mikoa ya Kanda ya Ziwa. Ukweli baadhi ya chakula kilichopo kwenye maghala na mashine za kukoboa mpunga ni chakula cha watu binafsi ambao wengi ni wakulima waliopata mavuno mengi mwaka jana, ambao ni kama asilimia15 ya wananchi hao wa vijijini na wakulima hawa ama hawataki kuuza kwa hofu ya njaa au wanasubiri bei zaidi isiyojulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu chakula hiki mpaka leo ni kingi sana kama kingekuwa cha Serikali lakini ni cha watu binafsi, kwa hiyo huenda hata takwimu zikatofautiana kadri muda unavyoenda. Itakumbukwa hata wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais Wilayani Kahama nilimwomba awaruhusu wauze mchele wao nje maana soko la ndani lisingeweza kununua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna asilimia 25 ya wananchi ambao wanategemea kuuza mifugo yao ili wanunue chakula, lakini bei ya mifugo haipo kupelekea kurudi na mifugo yao toka minadani au magulioni bila kuuza na kuongeza hofu kubwa ya maisha kwa wananchi hawa hasa ikizingatiwa wanakabiliwa na ukame pia kwa ajili ya malisho na maji kwa ajili ya wao na mifugo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 60 ya wananchi ambao wakiwemo watoto, wazee, wajane na watu wenye ulemavu mbalimbali na watu ambao ni maskini kabisa kundi hili ndilo linahitaji msaada wa dharura. Ni ukweli watu hawa walipata mavuno mwaka 2015/2016 lakini baada ya ukame wa mwezi wa Novemba – Desemba na Januari kuwa mkubwa ikapelekea mavuno machache na viwavi jeshi vikala kidogo kilichokuwepo kuwapelekea kupitia kipindi kigumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa historia na jiografia ya maeneo haya hakuna sehemu yoyote wanaweza kupata pesa ili waweze kununua chakula hata cha bei nafuu, hawana mifugo, hawana ndugu wa mjini ambao wanaweza kuwasaidia na hakuna hata sehemu ya kufanya kibarua ili waweze kupata pesa wanunue chakula, ikizingatiwa watakuwa kwenye njaa kuanza Juni – Januari ambapo kama hali ya hewa itabadilika katika maeneo haya ambayo ni karibu miezi saba mpaka nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri anapofanya majumuisho yake aje na jibu sahihi ili Wabunge wanaotoka maeneo haya yaliyoathirika na ukame tuwe na majibu sahihi kwa watu wetu, vinginevyo nitakamata shilingi ya bajeti.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza niwapongeze Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, rafiki yangu daktari, ingawaje sasa hivi haonekani toka amepata uwaziri. Nawapongeza sana pamoja na wafanyakazi wa Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, dhahabu ni kama ilivyo petrol na diesel, sisi kwa sasa hivi tunavyo-treat dhahabu tunai-treat kama bidhaa ya viwandani. Utajiri wa Waarabu ni pale mafuta yanapopanda, anayenufaika ni nchi ile kwenye ile difference ya kile kilichopanda. Bei ya dhahabu kabla vita ya Ukraine haijaanza ilikuwa ounce moja dola 1,800, lakini siku bomu limedondoka moja bei iliruka mpaka 2100, ongezeko la dola 300 ambayo sawasawa na dola 10 kwa gramu.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu hapa ambayo najaribu kuijenga, je, hiki kilichoongezeka ni mali ya nani? Kwa sababu yule mwenye mgodi alikuwa anachimba na anapata faida na hiki kilichopanda hakikupanda kwa gharama ya uzalishaji, kilipanda kwa hofu iliyoingia duniani. Kwa wenzetu fedha hizo ni mali ya Serikali asilimia 100. Nasema hivyo kwa sababu mwenye mgodi hawezi kulalamika kwa sababu yeye gharama ya dhahabu haitokani na bei unayouza, inatokana na wewe unavyoendelea. Kwa hiyo bomu lilipodondoka bei ya dhahabu ilipanda muda uleule na tofauti iliyopo hapo kwa uzalishaji wa dhahabu kwa Tanzania ambao ni karibu tani 45 kwa mwaka, ni sawasawa na dola milioni 40 kwa mwezi. Pesa hizo kwa rate ya leo ni sawasawa na bilioni 200 kwa mwezi. Ni tofauti ya bei iliyotokea baada ya bomu kudondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzetu Waarabu ndicho kinachowapa utajiri, hatajiriki BP, anatajirika yeye mwenye mali. Ni hesabu rahisi haiitaji elimu kubwa sana; ukiweka mpunga kwenye mashine ya mtu au ukaweka alizeti ukasuburi kuja kukamua, inapopanda bei ya alizeti anayenufaika au mpunga anayenufaika ni yule mwenye mpunga si mwenye mashine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuwaombe wenzetu wa wizarani kwasababu elimu hii ya madini najua wakati mwingine tukiongea elimu kuna kuwa na mvutano. Elimu hii ya madini ni mpya kwenye Idara zetu na kwenye shule zetu, kwa hiyo tuwaombe watalaam kama wanaweza kushauriana na hao wenye mgodi na hawawezi kukataa na hata tukiziacha hizi pesa, si kwamba mwenye mgodi atanufaika zitatengenezewa matumizi mengine ambayo yatazamia humo ndani. Kwa kawaida hizi pesa ni mali ya Serikali, zinaweza zikatusaidia mno. Zinatosha kabisa kutibu watu wetu bure kwa mwaka na kuwapa chakula cha mchana hata watoto wetu wa shule. Tuwaombe sana wenzetu wa madini wafikirie sana suala hilo kama wanaweza kulipeleka linaweza likatusaidia hasa sisi tunaotoka maeneo ya madini.

Mheshimiwa Spika, nilitaka kuchangia hayo tu. Baada ya mchango huo, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza natoa shukrani nyingi kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika Wizara ya Elimu.

Kwanza napenda kutoa shukrani nyingi kwa Serikali kwa kutoa elimu ya bure kutoka darasa la kwanza mpaka la kumi na kbili. Mpango huu wa elimu bure umetusaidia sana kupunguza kero nyingi majimboni kwetu pia Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya Tanzania kama haitafanyiwa mabadiliko makubwa itaendelea kuwa chanzo cha mateso, umaskini kwa wazazi, watoto na kurudisha nyuma maendeleo ya nchi yetu. Wakati wakoloni walipoleta elimu zaidi ya miaka 100 iliyopita walikuwa na maana nzuri sana, leo baada ya mabadiliko makubwa ya dunia, uchumi na teknolojia kwa ujumla wake ni vigumu sana kuendelea na mfumo wetu wa elimu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano kwa nchi ya Uingereza; wanapomaliza wanafunzi mfano, milioni moja kutakuwa na retirement ya wafanyakazi karibu laki tisa au laki tisa na nusu ambao ni asilimia 90 mpaka 95. Kwa hiyo, wale wanafunzi laki moja ambao watakuwa hawana ajira watakuwa chini ya Serikali wanaweza kulipwa na kutafutiwa kazi polepole.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wetu, wakimaliza wanafunzi milioni moja kutoka chuo na shule zote watakaopata kazi ni wanafunzi 50,000. Kwa maana hiyo ajira yetu ni asilimia tano peke yake ya wanafunzi. Kwa tofauti hii ya uwiano wa ajira kati ya waliotuletea mfumo huu wa elimu na waletewa, hata ikitokea miujiza hatuwezi kutengeneza ajira hata kwa asilimia 20. Ni jukumu la Wizara kuchukua mawazo ya Wabunge yanayoweza kufanyiwa maboresho ili kulitatua hili tatizo ambalo ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tunaotoka Mikoa ya Kanda ya Ziwa tungeomba kutoka darasa la kwanza mpaka kidato cha nne kwa shule za kutwa tupewe elimu ya kawaida na tupewe elimu ya mazingira yetu. Kanda ya Ziwa tuna shughuli zetu za kawaida kama ufugaji, uvuvi, biashara, madini, tungeomba Wizara ya Elimu itupatie elimu hii kutoka darasa la kwanza ili mtu anapomaliza form four awe ana-balance ya elimu mbili. Kwa hiyo, ataamua mwenyewe aendelee kwenda kwenye ajira ya Serikalini au sehemu nyingine au arudi akajiajiri kuliko mtindo wa sasa hivi baada ya mtu kumaliza university anarudishwa nyumbani. Akirudi nyumbani anakukuta wewe mzee umezeeka, huna kitu cha kufanya anakuja na karatasi inayoitwa degree. Tatizo hili ni tatizo la Watanzania wote, kila mtu ni mwathirika wa hili tatizo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunamuomba Waziri ajaribu kuangalia upya muda wa kukaa shuleni. Kama hatuna ajira ingekuwa vizuri mtoto amalize university akiwa na miaka 15 au 17 ili awakute baba na mama yake at least wana nguvu kwa maana hakuna kazi ili waendelee pamoja akiwa bado mdogo ni rahisi kufanya naye kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna tatizo la watu wa vyuo vikuu; vyuo vikuu vinaendesha nitaita kama aina ya utapeli mamboleo. Wanachukua pesa kwa wananchi, wanalazimisha wananchi kukopa, wanachukua pesa, shilingi milioni 10 mpaka shilingi milioni 30, baada ya miaka mitatu wanakurudishia mtoto ana karatasi inaitwa degree. Wao ndiyo kiwanda pekee kilichobaki duniani ambacho hakiwezi ku-suffer, viwanda vyote vinateseka sasa hivi lakini vyuo vikuu hakuna mahali vinateseka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wizara ilete sheria hapa ili wanapotaka kusajili hao wanafunzi waeleze kazi walizonazo ili wao waende kwa waajiri waende wakatafute hizo kazi kabla hawajasajili wanafunzi. Waeleze mshahara ndiyo waseme sasa lipa kiasi hiki mtoto wako atakwenda kufanya kazi hapa. Hii itasaidia ndugu zetu maprofesa na wamiliki wa vyuo kulijua soko la ajira, itabidi wakakutane na waajiri. Kwa sasa hawakutani na waajiri, wao wanatayarisha wanafunzi wanaacha wazazi na wazee wote nyumbani wanakuwa maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, usukumani tunakaribia kumaliza ng’ombe, tunalipia vyuo tunabaki na karatasi inayoitwa degree, lakini ukienda kwa mwajiri akiikataa ina maana hiyo degree ni valueless (haina thamani yoyote). Kwa hiyo, tungemuomba Waziri alete sheria hapa Bungeni ili vyuo vikuu viweze kubanwa na vyenyewe viende vikatafute ajira, badala ya mtindo wa sasa hivi wa vyuo kutumia nguvu ya Serikali na mawazo ya kusema elimu ni ufunguo wa maisha, matokeo yake sasa elimu ni kibano cha maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea kidogo suala la VETA; humu ndani wote tuna magari, lakini sijasikia mtu yeyote anasema anapeleka gari yake VETA, wote tunauliza wapi ambapo kuna garage nzuri ya Toyota tunaambiwa ipo Mwembeni, tukifika pale Mwembeni hatuulizi cheti chochote, ningemuomba Waziri awafikirie sana watu wa garage maana yake ndio wanaofanya kazi kubwa kwa sasa hivi. Kama wao anaweza kuwa-indicate kama VETA ili wanafunzi wetu wakaenda kwenye garage za Miembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzuri ni kwamba garage hizo hazina masharti yoyote ya kusoma, unaweza kusoma miezi sita kama umeshaelewa unaweza kuendelea na shughuli zako. Tofauti na sasa hivi unapeleka mtoto VETA kujifunza kupaka rangi miaka mitatu, fundi bomba miaka mitatu akirudi anakuta teknolojia ya bomba imeshamalizika inakuwa hakuna chochote. Hawa wakiona ametoka VETA wote huku mtaani hawamtaki, wanasema huyu ni soft, lakini anayetoka kwenye garage anapokelewa vizuri sana maana yake ni practical. Tunaweza kuwapeleka kwenye maeneo ya sofa, maeneo mengi sana ambayo yapo sasa hivi, yanatosha kabisa kuweza kusaidia VETA badala ya mtindo wa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo, namuomba Waziri, pamoja na yote hayo, anisaidie kwenye Jimbo langu la Kahama shule Nne za sekondari ambazo zimekuwepo kwa muda mrefu kuwa High School.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ni huo kwa leo, nashukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nitaenda moja kwa moja kwenye Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri yangu ilipata hati safi kwenye ukaguzi wa CAG vile vile kwenye mwenge tulikuwa washindi wa pili au wa tatu. Lakini kitu cha kushangaza ripoti ya Mkaguzi wa Ndani wa Halmashauri inaonyesha tuna upotevu wa zaidi ya milioni 200 na zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najaribu kujiuliza hapa kwamba inawezekanaje tuna hati safi kwenye mwenge tumekuwa wa pili au wa tatu lakini mkaguzi wa ndani kwenye ripoti ambayo ninayo hapa anaonyesha tuna upotevu wa zaidi ya milioni 200 na zaidi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi Mkurugenzi wetu wa Halmashauri ameendelea kuwaburuza Madiwani kwa kutumia ubabe kiasi ambacho ameweza kuidhinisha ujenzi wa jengo la mamalishe lenye thamani ya shilingi milioni 200. Jengo hili kwa gharama ya shilingi milioni 200 lina mapato ya shilingi 120,000 kwa mwezi. Kwa hiyo faida ya kurudisha jengo hili litachukua zaidi ya miaka 200. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa namwomba waziri atakapokuwa anafanya majumuisho ajaribu kuangalia kama Serikali inakopa pesa, pesa hizo hizo milioni 200 ilizokopa kwenye mabenki ya ndani kwa riba ya asilimia kumi yenyewe italipa milioni 20. Ni vipi imeipatia Halmashauri ikajenga jengo la milioni mia mbili itapata return baada ya miaka 200 na itapata shilingi milioni 1.4 kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha ubadhirifu huo unaoendelea kwa hao watu wanaitwa wateule wa Rais, Mkurugenzi huyu mpaka leo amekataa kutoa statement za benki, Mkuu wa Wilaya hawezi kumhoji, TAKUKURU hawezi kumhoji, Mkuu wa Mkoa hawezi hata sisi kamati ya fedha amekataa na kichekesho hapa ninapoongea anaendelea kupiga machinga wote wa Kahama. Namshukuru Mkuu wa Polisi amekataa kutoa polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mji wetu wa Kahama watu walioajiriwa hawafiki watu 200, na mji ule una watu zaidi ya laki tano, ni kweli watu hawa watafanya shughuli gani? Hata hivyo Mheshimiwa Rais alisharuhusu machinga na watu wa kawaida waendelee na shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri Jafo wakati anafanya majumuisho ajaribu kutueleza tutafanya nini au tushitaki wapi sisi? Maana hatuna sehemu yoyote ambayo tunaweza kulalamikia. (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naipokea hoja yako vizuri nafikiri Mheshimiwa Jafo uko hapo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli sisi ni Wabunge, lakini mtu ambaye anasema yeye ni mteule anapojaribu kuwa- disturb watu waliokupigia kura anatupa sisi wakati mgumu sana. Tunajaribu kila namna kutafuta pesa kutoka kila kona, ili tusaidie watu wetu, lakini mtu anafika anakataa au ana- misuse hizi pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna ongezeko la wanafunzi kwenye kidato cha kwanza zaidi ya asilimia 200; kwenye darasa la kwanza tuna ongezeko la asilimia 200 pia, tuna upungufu wa matundu 2,000 ya choo, lakini Mkurugenzi huyu amechukua pesa hizo milioni 200 amepeleka kwenye jengo la mama lishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hivi ninavyoongea Mheshimiwa Jafo ulipokuwa Naibu Waziri ulitoa agizo kwamba, wakati Wabunge wako Bungeni Kamati za Fedha zisikae, lakini yeye anaitisha Kamati ya Fedha kesho, ameongeza shilingi milioni 40 tena kupeleka kwenye jengo hili kwa ajili ya kuweka vigae. Kwa hiyo, naomba sana mtusaidie maeneo haya ni maeneo ambayo yanatupa matatizo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia tu naomba Mheshimiwa Jafo na Mheshimiwa Kakunda kwa kuwa mlifika Kahama mtufikirie sana suala letu la Manispaa. Ni kweli mji wetu umekua, mmeuona kwa macho na matatizo tuliyonayo. Mkitusaidia Manispaa itatusaidia vile vile kwa tatizo la barabara ambalo kwa sasa ni tatizo letu kubwa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi kuchangia Wizara hii ya Viwanda na Biashara. Nitaanza upande wa viwanda na uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili suala ambalo linaendelea sasa hivi kwa Kiswahili linasema kuongeza thamani au kwa Kingereza ku-add value. Suala hili kama hatukulifanyia utafiti wa dhati litatuletea mtafaruku mkubwa. Maana yangu kusema hivyo ni kwamba, kila mwenye kiwanda sasa hivi anapigania kuzuia wananchi wasiuze mali zao akiwa anasema yeye yupo tayari kununua mali yote na kui-add value. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano. Hapa tunakatazwa kuuza mahindi nchi za nje tunaambiwa tuuze sembe lakini watu wa Kongo sembe wanachanganya na muhogo, sasa utawauziaje sembe na wenyewe wakachanganye muhogo, wanakwambia wanataka mahindi ili wakasage waweke muhogo. Kwa kuwa Waziri yuko hapa aliangalie kwa makini sana suala hili, kama mtu anasema anataka ku-add value ni lazima aoneshe uwezo wa kiwanda chake ataweza kweli kununua mali za Watanzania ili watu wasikae na mali zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano kwenye ngozi. Sasa hivi karibu ngozi zote zinatupwa, zimezuiwa na zimewekewa export levy ya 80% na indication price iliyowekwa na TRA ni senti 58 ya Dola ambayo ni Sh.1,300 lakini bei ya ngozi leo duniani ni senti 35 ambayo ni Sh.800. Itawezekana vipi sasa mtu alipie Sh.1,300 auze Sh.800? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumesaini mkataba na Uganda na Kenya kwenye hilo suala la ngozi. Wenzetu Waganda na Wakenya wana-under value invoice, wanalipia kwa bei chini na kununua mali zetu, ni kwa nini na sisi wananchi wetu wasiruhusiwa kuuza mali zao ili kuondoa huu mtafaruku ambao unaendelea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaungana na Wabunge wenzangu kwenye suala hili la Liganga na Mchuchuma ingawaje mimi mtizamo wangu uko tofauti kidogo. Mtizamo wangu mimi ni kwamba, madini haya kwa utafiti wa wataalam wetu wanavyosema yako mengi kiasi cha kutosha miaka 100 lakini miaka 100 kwa dunia inavyokwenda haraka ni kweli teknolojia hiyo au chuma hicho kitakuwa kinatakiwa duniani. Kwa nini tusiwe na option mbili, tukawa na option ya kuuza udongo wa chuma kama ulivyo na tukawa na option ya kuyeyusha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya analysis ya madini yaliyomo mle ndani nchi nyingi duniani wakati bei ya chuma au madini fulani yanapanda wanauza kwa ajili ya kupata pesa muda ule na kujikimu. Sasa hivi hapa kwetu tunalia kwamba, hatuna pesa ya maji lakini tuna mlima zaidi ya miaka 50, kuna ubaya gani kufanya analysis na baadhi ya mawe yale yakaendelea kuuzwa ili tupate pesa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwenye Jimbo letu la Kahama au Wilaya yetu ya Kahama na Mkoa wa Shinyanga mwaka huu tuna mavuno mazuri sana ya mpunga. Tunamwomba Mheshimiwa Waziri hili neno la add value aliangalie. Sisi tunataka kuuza mpunga au mchele kwa Waganda lakini tunabanwa na sheria inayosema huwezi kuuza mpunga lazima ukoboe mchele, lakini wakati unasubiri kukoboa mchele hilo soko litakuwa linakusubiri kweli kule Uganda? Haiwezekani. Ni lazima Mawaziri wafikirie sana suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda kwenye suala la biashara. Kwenye mkutano wa Mheshimiwa Rais ni kweli mambo mengi sana yalijitokeza pale. Ukiangalia maswali mengi ya wafanyabiashara ilikuwa ni kwenye tatizo la Sheria ya Importation na Sheria ya Kodi ya Mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Importation inatusumbua, sisi tunatumia tarrif ambayo haisumbui sana ukienda kwenye vitu kama mafuta ta dizeli, sukari, simenti na vinywaji kwa kuwa hawa wanatumia ujazo au kilo lakini unapokwenda kwenye item ndogondogo, nitatoa mfano wa item moja, kwa mfano wewe ume-import glass, glass kwenye tarrif inaitwa glassware, lakini kuna glass ya Sh.10,000 na ya Sh.1,000 lakini TRA ata-pick glass ya Sh.10,000 kuku-charge wewe wa glass ya Sh.1,000/=. Kwa hiyo, tunamwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kuwa yuko hapa ni miongoni mwa kero nyingi sana ambazo wafanyabiashara wamezionesha wakati wa kufanya importation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna tatizo kubwa sisi tunaotoka mikoa ya mpakani. Kuna hii sheria mpya ya ku- declare pesa. Wananchi walioko Kongo, Burundi, Uganda wanataka kuja kununua mali kwetu Mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Geita. Haiwezekani mtu atoke Uganda au atoke Kongo afike Mutukula aoneshe Dola zake 50,000 apande basi, ni kitu ambacho hakiwezekani hata iweje. Tumeshuhudia wote hapa mtu anatoka kuchukua pesa pale Mlimani City anavamiwa anauawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri wa Fedha kwa kuwa yuko hapa alifikirie, hili neno tume-copy kwa Wazungu, kwao ni sawa, London uki-declare hakuna mtu atakuvamia lakini ku-declare kilometa 300 upite porini ambako mpaka mabasi yanafanyiwa escort na wewe ulionesha dola, tumekwama kabisa watu wa nje wamekataa kuja kununua mali kwetu kwa sababu hiyo, hawawezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia nchi hizo ni zile ambazo hazina mfumo wa kibenki, Kongo hakuna benki, Burundi kuna vita, watu hao wote wanatembea na cash. Nafikiri Waziri wa Fedha kwa kuwa yuko hapa ajaribu sana kulifikiria suala hili ambalo linatusumbua sana. Sisi Mwanza tunauza samaki, mchele na vitu vingi lakini mpaka sasa tumekwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia kwa kuwa na Waziri wa Nishati yuko hapa tungeomba sana wenzetu wa TANESCO waruhusu, kama walivyoruhusu kwenye transformer, kwa wafanyabiashara hasa wanaotaka kuanzisha viwanda kama wanaweza kuvuta umeme kwa gharama yao halafu wakawarudishia wakati wa bili inapoanza. Kwa kuwa, yeye sasa hivi analalamika kwamba hana pesa ya kununua nguzo au vifaa vya umeme itasaidia watu wanaotaka kuanzisha viwanda waweze kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango huo, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi kuchangia Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara hii inaonekana ndiyo Wizara ambayo itakuwa ngumu safari hii kwenye Bunge letu. Namuomba ndugu yangu Mheshimiwa Mpina ambaye anatoka eneo la wafugaji wa ng’ombe, tunaotoka maeneo ya ufugaji tunaomba hizi ranchi kwa mara ya kwanza ziruhusiwe wananchi wetu waweke ng’ombe mle, walipie officially Serikalini ili Serikali na Wizara yake ipate pesa badala ya sasa hivi pesa hizo zinaenda kwa watunzaji wa hifadhi hizo. (Makofi)

Mheshmiwa Spika, leo tunahangaika watu wanachukua ng’ombe kutoka Usukumani kwenda mpaka Lindi, lakini tuna Ranchi ya Mwabuki ambayo inaweza kuchukua ng’ombe zaidi ya 500,000 mpaka milioni moja. Wizara kama itaruhusu ng’ombe laki tano au milioni moja wakakaa pale Mwabuki, kutajengwa automatically viwanda vya maziwa, vitajengwa viwanda vya nyama bila hata shuruti ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, ranchi hiyo haina ng’ombe zaidi ya 500. Kuna fisi, kuna nguruwe, hakuna kitu chochote. Ingekuwa vizuri Wizara ikaanza kuchukua action.

Mheshimiwa Spika, tuna pori ambalo linatokea Kahama mpaka Kigoma, Mheshimiwa Dotto alikuwa analia sana mara nyingi maana yake amepakana nalo. Pori hilo lina urefu wa kilometa 400, upana kilometa 250. Halina wanyama, siyo National Park kwamba watalii wanaenda, kwa nini Serikali isitoe hata asilimia kumi ikaruhusu watu wakaweka ng’ombe zao na wakalipia officially Serikalini na ikapata mapato na wananchi wetu wakapata malisho.

Mheshimiwa Spika, nawalaumu sana wataalam wa mazingira, ni kweli wanatupotosha na ni waongo. Ng’ombe hali miti wala hali udongo, ng’ombe anakula nyasi. Ng’ombe akila nyasi kwenye pori wakati wa kiangazi moto unapokuja unainusuru ile miti. Wataalam wanatuletea maneno ya Ulaya ya uongo kwamba ng’ombe akiingia kwenye lile pori ataharibu, ataharibu nini.

Mheshimiwa Spika, pori lile ni nusu ya nchi ya Uganda. Ni kweli ng’ombe waliopo pale wanaweza kudhuru nini? Leo wako ng’ombe pale wanatozwa pesa na watu wanapata pesa hakuna kitu chochote. Ni vizuri Mheshimiwa Mpina Serikali yako ili ipate pesa, ruhusu watu wachunge officially, uwatoze pesa officially, lakini wananchi wetu watapata manufaa na maendeleo pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakwenda kwenye suala la uvuvi. Mimi kwangu sina ziwa wala mto lakini makao yangu ni Mwanza. Ukweli hali inayoendelea kule Kanda ya Ziwa ni hatari na sijawahi kuiona kwa zaidi ya miaka 30. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mji wa Mwanza, ukiondoa kilimo, ukaondoa na dhahabu kinachofuata ni samaki. Leo hali iliyopo kule ni hofu, sijawahi kuiona kwenye maisha yangu. Mwananchi wa kawaida anakatazwa kubeba samaki kwenye pikipiki anakimbizwa, kwenye baiskeli anakimbizwa, matokeo yake haijulikani hasa samaki wanatakiwa kupigwa marufuku au inatakiwa nini. Kama kuna tamko la Serikali, basi Serikali itamke kwamba imesitisha ulaji wa samaki kwa muda hadi hapo itakavyojulikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wavuvi hawa wanaosemwa, kweli siungi mkono uvuvi haramu lakini hawezi akakosea mtu mmoja tukaamua kwenda kupiga watu wetu kwa model hiyo, kwa kweli nakataa! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lawama kubwa naitupa kwa wataalam wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Nchi zinazoongoza duniani sasa hivi kwa uuzaji wa samaki, siyo nchi zenye maziwa wala bahari, nchi ya Thailand ndiyo inazoongoza kwa samaki, Serikali inatoa vifaranga milioni 200 kila mwezi, inawapa raia wake wafuge ama kwenye malambo, mabeseni, ndoo, baada ya miaka miwili, samaki walio nchi kavu ni wengi kuliko waliopo ziwani. Kwa matokeo hayo, Mheshimiwa Mpina na wataalam wake ambao tunawaita wachawi wa kizungu, maana wasomi wenzetu tunawaita wachawi wa kizungu, wenyeji wanaitwa wachawi wa kienyeji ni kweli!

Mheshimiwa Spika, viongozi wetu ambao ni wasomi, msomi kugeuka kuwa mgambo kwenda kupiga raia inahuzunisha sana. Kazi hiyo ilitakiwa ifanywe na mtu ambaye hana degree, siyo kama Maprofesa alionao nao Mheshimiwa Mpina. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo kama wataalam wasingetengeneza mayai ya kizungu, leo mayai ya kienyeji yangekuwa shilingi 5,000. Wataalam wasingetengeneza kuku wa kizungu, leo kuku wa kienyeji angekuwa shilingi 50,000. Wenzetu wasomi wao walikaa wakafikiri, badala ya kugombana na wananchi wakaja na solution, solution hiyo ndiyo inayotufanya leo hatujaamka kwenda kugombana na wananchi wanaofuga kuku na mayai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba wataalam wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wazalishe samaki, warudishe mbegu za samaki kila mwezi ziwani, wawagawie na wananchi mbegu za samaki bila kupeleka maneno yao ya mazingira, bila kupeleka maneno yao ya uongo ya mazingira, uongo mtupu! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namuomba Mheshimiwa Mpina ajaribu kupunguza jazba. Ni kweli wananchi kule hawana nyavu. Nyavu zinazotengenezwa zinatoka Kiwanda cha Sunflag, kiwanda hiki kinatengeneza vyandarua hata kama tutaficha, lakini kweli nyavu hizo zinaweza kuvua samaki? Vyandarua haviwezi kuvua samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namuomba sana Mheshimiwa Mpina, asituone Wabunge kama ni watu wabaya, wote tunategemea samaki, tuna biashara zetu kule ambazo siyo samaki lakini zina uhusiano na samaki, hatuwezi kukataa, maeneo yetu yote yale yanahusika na samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwangu Kahama samaki wanaliwa. Population ya watu imeongezeka, ulaji wa samaki umeongezeka, haiwezekani wataalam wetu, watu waliosoma kwa gharama kubwa wanang’ang’ana tu kupiga watu badala ya kung’ang’ana kutafuta ufumbuzi! Kama ndugu zetu wazungu walivyoleta ufumbuzi wa kutengeneza mayai, wakatengeneza na kuku wa kizungu, leo hatuna mgogoro unachagua mwenyewe unachotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kweli leo Maprofesa wazima wanaungana kwenda kupiga watu! Uzuri na Mheshimiwa Profesa Kabudi kama yuko hapa ingekuwa ni wanasheria au madaktari wangesimamishwa kwa ajili ya degree zao lakini sijui kwa degree zingine kwamba sheria inasemaje kama mtu aliyesoma anapoharibu heshima ya degree hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo yote naomba vilevile kwa Mawaziri ambao tunaendelea na migogoro mingi hapa, kwa zile sheria ambazo Mawaziri wanaziona kama zina matatizo, wazilete tena sheria hizo Bungeni zifanyiwe marekebisho kama Mheshimiwa Rais anavyofanya. Mheshimiwa Rais juzi alifanya mabadiliko akaleta Sheria ya Madini, amesema iletwe Sheria ya Mafuta ifanyiwe mabadiliko, Mheshimiwa Luhaga Mpina na Mawaziri wengine ambao wanaona kuna matatizo, leteni sheria hizo hapa zifanyiwe mabadiliko ili kuondoa ugomvi na wananchi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. JUMMANE J. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye bajeti yetu hii ya 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo mawili au matatu kama muda utaniruhusu. Suala langu la kwanza alijaribu kuliongelea hapa Mheshimiwa Ngeleja. Suala hili la dhahabu tumekuwa tukiliongea leo mwaka wa tatu toka tumeingia hapa Bungeni, sijaelewa ni kwa nini Waziri Mpango hataki kulielewa. Mara ya kwanza mimi nilikuja na hoja ya one percent kwa dhahabu kwa watu wanaofanya export. Tuliongea na Mheshimiwa Mpango lakini baadaye sikupata jibu kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhahabu ni sawasawa na dola, sijaelewi kwa nini tunapuuza dhahabu ya wachimbaji wadogo ambayo ni karibu ya asilimia 70 ya dhahabu yote ya Tanzania na leo migodi yetu mikubwa imefungwa. Sisi tunaotoka maeneo hayo ya dhahabu tunaifahamu dhahabu vizuri sana. Benki Kuu ya Tanzania ilianza kununua, kama alivyosema mwaka 1991/1992, baadaye ilisimama baada ya matatizo yaliyotokea pale kwamba uaminifu uliokuwepo haukuwa mzuri kati ya wafanyakazi wa Benki Kuu na wafanyabiashara waliokuwa wanapeleka dhahabu pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukiangalia trend ya dhahabu duniani, kama alivyosema Mheshimiwa Ngeleja, kwamba tangu mwaka 1999 kwa mfano dhahabu imekuwa ikipanda kwa speed nzuri sana. Serikali ingekubali kununua dhahabu kwa ushindani kwa bei ya soko la dunia kwa shilingi za Tanzania ingeweza kupata faida kubwa na ingeweza kuifanya pesa yetu kuwa imara. Sasa hivi kinachofanyika ni kwamba, Serikali inapotaka kulipa madeni lazima ichukue pesa za shilingi ika-source dola, lakini ingekuwa inanunua dhahabu ingeuza kipande cha dhahabu wakati inapotaka kulipa deni. Hii ingesaidia shilingi yetu vile vile isiweze kuporomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nafikiri kinachotusumbua hapa huenda hii dhahabu ya local kwa kuwa haimo kwenye mitaala ya shule, labda kwa kuwa haiko shuleni kwa watalaam wa uchumi inawapa kigugumizi; kwa sababu Waamerica na Waingereza wanaotoa elimu hawana hiyo dhahabu ya kuokota mitaani. Kwa hiyo kuna uwezekano mkubwa kwamba, kila ukimwambia mtu ambaye hafahamu anaona unaongea kitu ambacho si sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mwaka 1999 kweli dhahabu ilikuwa dola 270 kwa Ounce, ambayo ni kama dola nane ama tisa; leo iko dola 1400 ambayo ni takriban dola 50. Kwa hiyo imepanda kwa asilimia 800. Pesa ya Tanzania mwaka 1999 ilikuwa 1,300 leo ni 2,300, pesa ya Tanzania ime-depreciate kwa asilimia 80. Kwa hiyo kama tungekuwa na stock ya dhahabu deni la Taifa tungelifuta lote mara moja na tusingekuwa na deni lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunamwomba Mheshimiwa Mpango ajaribu aidha atuite watu tunaotoka maeneo ya madini, tujaribu kuongea na watalaam wake kama kuna sababu hasa, kwa maana hatupi jibu ni kwa sababu gani. Leo dhahabu yetu Uganda wana-charge 1.5 percent kwa export levy, Burundi 1.0 percent, Rwanda 1.0 percent; na watu hawa hawana mgodi hata mmoja na wote tuko Jumuiya ya Afrika Mashariki. Sisi tunaletewa plastic na Wachina, sasa itawezekanaje? Sisi tuna kiwanda cha kuchapa dola, dhahabu ni dola, ni kama una kiwanda cha kuchapa dola, hutakiwi hata kufikiria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo indication ya bei ya dhahabu duniani inaonekana kwamba itaendelea kupanda; nitatoa sababu tatu ambazo zinaonesha itaendelea kupanda. Sababu ya kwanza, ni kuwepo kwa sarafu mpya duniani; kuna sarafu ya Euro, kuna sarafu mpya ya China ambayo imekuwa imara, kuna sarafu mpya ambayo inatarajiwa ya nchi za Brazil, South Afrika na nchi za Asia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile dhahabu sasa hivi imeanza kutumika kutengeneza kwenye komputa na laptop, kiasi ambacho sisi ambao tunayo dhahabu, tunayo chance nzuri zaidi ya kupata faida kutokana na dhahabu. Kwa hiyo namwomba sana Mheshimiwa Waziri na Waziri wa Madini wajaribu, kama watalaam wao wanakuwa na kigugumizi kwa ajili ya matatizo yaliyotokea mwaka 1992, teknoloji ilikuwa bado, leo teknoloji ya dhahabu ni ya kugusa simu unajua ina percent ngapi ya dhahabu ndani yake; tunaomba wasiwasi huo uondoke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunajenga reli kwenda Mikoa ya Mwanza na kwenda Mikoa ya Kigoma. Wajerumani wakati wanajenga walikuwa wakati huo huo wanaandaa na mazao ya kwenda kubebwa na treni ile. Kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Mpango awekeze kwenye mazao ambayo treni standard gauge itakapokuwa imefika kule Kigoma na kule Mwanza licha ya abiria kuwe na mazao ya kuweza kubeba kurudi nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa idea ndogo tu, kwamba Malaysia kilichofanya wakafanikiwa kwenye michikichi ni kwamba walikuwa wanampa mtu mche wa mchikichi halafu kila mwezi wanamlipa pesa yule mtu. Baada ya miaka mitatu mchikichi ilivyoanza kutoa matunda yule mtu analipa. Kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Dkt. Mpango na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo aweke pesa pale, awapatie wananchi wetu michikichi na mikorosho awape Sh.1000 kila mche, gharama yake itakuwa Sh.40,000 peke yake kwa mche mmoja, lakini baada ya miaka mitatu atakuwa na miche mingi ya korosho nyingi na michikichi mingi. Kwa hiyo treni yake itakapofika Kigoma atakuwa na mizigo ya kurudi nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia tu, ningemalizia kwenye kodi ya viwanja na majengo. Tanzania ni nchi pekee ambayo ina-charge kodi ya viwanja na majengo kwa kumfata mtu. Nchi zote duniani zinatumia kwenye bill ya maji au umeme. Mimi kama kodi ya kiwanja ni Sh.24,000 au kodi ya jengo ni Sh.24,000 tunagawa kwa 12. Kwenye bill yangu ya maji unaleta elfu mbili ambayo inakuwa indicated pale kwenye bill ya maji au ya umeme. Nafikiri Mheshimiwa Waziri wa Fedha anaweza akalichukua hili litamsaidia zaidi na hatakuwa na sababu yoyote ya kushinda kutwa nzima na majembe Auction Mart, kamata huyu, funga huyu, inaweza ikatusaidia sana sana, Mheshimiwa Waziri wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo naomba nihitimishe mchango wangu kwa kuongelea suala la bandari. Bandari yetu ya Dar es Salaam inafanya kazi vizuri. Hata hivyo namwomba Mheshimiwa Dkt. Mpango aangalie zile bidhaa ambazo zinakwenda nchi za jirani, aongee na wafanyabiashara wa Kariakoo kwamba kwa nini bidhaa hizi haziuzwi hapa, ili aone ufumbuzi. Kama zinaweza kuteremshwa bei na hazina madhara kwa viwanda vya Tanzania ni vizuri ikafikia upya suala la kupunguza kodi juu ya bidhaa ambazo zinaweza kulipishwa ushuru hapa na wewe ukapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Madini
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakwenda moja kwa moja kwenye dhahabu. Katika Jimbo langu la Kahama ni miongoni mwa maeneo ambayo yana machimbo mengi sana madogo madogo, pamoja na mgodi mkubwa wa Buzwagi na jirani yangu Bulyanhulu. Kinachosumbua sasa hivi, kule ni Sheria ya Madini ambayo watu wa migodi mikubwa wanatumia sheria hiyo hiyo na wachimbaji wadogo wadogo wanatumia sheria hiyo hiyo. Sasa hivi wachimbaji wadogo wadogo, akitoa mifuko 10 ya mawe ya dhahabu, anatoa mfuko mmoja kwa ajili ya madini, mfuko mmoja kwa ajili ya TRA, mfuko mmoja kwa ajili ya Halmashauri na mfuko mmoja kwa ajili ya mwenye shamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu huyu akimaliza tena kusaga mchanga ule kwenda kutoa dhahabu analipa tena, mchanga ule tena ukienda kuchenjuliwa unalipiwa tena lakini huyu mwenye mgodi mkubwa akilipa ushuru wake yeye atarekebisha kwenye hesabu zake za TRA atapunguza zile gharama alizolipia, lakini huyu mchimbaji mdogo hana mahali ambapo anaweza kwenda ku-claim fedha aliyolipa. Matokeo yake inasababisha kuwa na rushwa na migogoro mingi sana maeneo yale. Kwa hiyo, tunaomba Wizara ya Madini ni vizuri ikaoanisha kati ya sheria ya migodi mikubwa na sheria ya wachimbaji wadogo wadogo ambao ni kama wakulima wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala hili la dhahabu nafikiri Serikali ingetamka wazi kwamba inataka kufanya kweli kazi ya dhahabu au ni kama tunataka kuruhusu uchawi lakini wakati tukiona bundi au fisi tunaogopa. Tanzania haina elimu ya biashara ya madini ina elimu ya miamba na tunachoibiwa na matatizo yetu makubwa yako kwenye elimu ya biashara ya madini ambayo haiko shuleni. Kwa hiyo, ni vizuri kama tunaamua kuruhusu biashara ya madini ionekane kwamba madini yameruhusiwa lakini hata tukiunda Tume 100, kama hatujasema wazi kabisa tunataka nini kwenye madini, bado tuna wakati mgumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi ya Uganda leo ina- charge service levy ya export 0.5%; Rwanda wana-charge 0.6%; Burundi 1%; Tanzania tuna-charge 14%. Mheshimiwa Waziri hata kama ni wewe unaweza ukapata dhahabu ya Sh.10,000,000 ukalipa Sh.1,400,000, inawezekana? Umechimba peke yako, ukapata dhahabu ya Sh.10,000,000 ukabeba kupelekea Serikalini Sh.1,400,000, inawezekana? Wafanyabiashara hawa wanafanya biashara ya madini zaidi ya miaka 10 hata mke wake hajawahi kuiona dhahabu, ni vipi Serikali inaweza ikachunga dhahabu kutoka Lindi mpaka Mara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii ya wachimbaji wadogo wadogo imeajiri zaidi ya watu milioni 5. Kwa hiyo, ni kweli Serikali kwenye kitabu inaonesha wamechangia asilimia 2 lakini tunapoteza zaidi ya tani 2 au 3 za dhahabu kila wiki. Kwa nini Serikali isiruhusu dhahabu ikawa 1% na alipe anaye-export ili hawa wachimbaji wadogo wadogo waondokane na huu msururu wa usumbufu walionao halafu wale wenye migodi mikubwa waendelee na procedure ya kawaida ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itasaidia hata jirani zetu ambao wana madini wanaweza kuyaleta hapa kwetu. Ni vizuri Serikali ikafikiria sana kuruhusu madini kutoka nje. Ni kweli tuna mikataba ambayo inasema lazima wapate certificate of original lakini ni kweli sisi tunapokea wakimbizi kutoka Congo, tunapokea kila aina ya matatizo kutoka nchi jirani, tunaweza kupata ebola, mbona tunakataa kupokea dhahabu na tuko tayari kupokea dola? Ni vizuri Serikali ikafikiria upya maana dhahabu haina alama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini watu hawa watanunua mali hapa na sisi tutapata pesa kutoka kwenye kodi. Sisi hatufanyi service Msumbiji, hatutengenezi barabara Congo ina maana tutapata pesa ya bure. Kwa kuwa Mwanasheria wa Serikali na Waziri wa Sheria wapo hapa waiangalie sana hii Sheria ya Madini ambapo dhahabu ni moja lakini inapatikana kutoka kwenye vyanzo viwili tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo, nahitimisha mchango wangu, naunga mkono hoja, ahsante sana
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Kamati hii ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu na Wataalamu wote, pamoja na Wabunge wote wa Kamati hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisiwe mchoyo wa fadhila, nachukua nafasi hii ingawa si Wizara yake, kumshukuru Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwa kuruhusu wachungaji na wafugaji pamoja na wakulima wanaokaa karibu na Hifadhi za Serikali kwa kuwaruhusu maeneo ambayo yana mapori ambayo hayana wanyama ili wananchi waweze kuyatumia wakati wa dharura, vilevile na vijiji 300 ambavyo vimeruhusiwa virasimishwe. Namshukuru sana kwa kupokea kilio cha wakulima na wafugaji cha muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naunga mkono mapendekezo ya Kamati, ila nina mawazo mawili/matatu ambayo yamo kwenye Kamati ningependa kuyafafanua na kuyaelezea vizuri, kama yataweza kuchukuliwa na kuwa msingi mzuri wa kuelekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, ni suala hili la Liganga na Mchuchuma. Suala hili la Liganga na Mchuchuma lina takribani zaidi ya miaka 50 na kinachoonekana tunaweza tukaenda tena miaka mingine 50 kama hatukupata ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chuma ni bidhaa kama bidhaa zingine na ndani ya chuma cha Liganga kuna mchanganyiko wa madini mbalimbali. Kwenye mkutano wa madini Mheshimiwa Rais alieleza na analysis zilizomo kwenye mchanga ule. Pendekezo tulilonalo ni kwamba Serikali ichukue analysis za gharama za uzalishaji kama itajenga Kiwanda cha Chuma, ichukue analysis ya mali iliyomo mule ndani ya chuma ione kama inaweza kuu-peg ule mchanga kwa bei ili wanunuzi waweze kununua kwa kulipia Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana ya kuongea hili ni kwamba, wenzetu Waganda leo wanachimba crude oil kutoka Uganda wanapeleka Tanga kupitia hapa lakini wananunua petroli na dizeli kutoka nje kwenda Uganda. Ni kwamba ndani ya crude ile kuna vitu ambavyo kama watachenjua hiyo crude oil kule Uganda hawawezi kuisafirisha au hawawezi kutumia ile material nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi kwa Liganga ni vizuri Serikali ikafikiria upya. Sababu nyingi za msingi ni kwamba chuma ni bidhaa kama bidhaa nyingine. Tunapoongea leo bei ya chuma duniani inaendelea kuanguka na hatujui ndani ya miaka kumi bei ya chuma itakuwaje maana chuma ni bidhaa ambayo inatumika na inakuwa recycle, sio kama chakula. Kwa hiyo hata kama tutang’ang’ania tunajua nini kitatokea baada ya miaka kumi. Ni vizuri Serikali ikafikiria kufanya analysis na kuanza kuruhusu chuma hicho Serikali iuze ili iweze kununua chuma kipya na kutumia au kupata pesa kwa ajili ya matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni kwamba ndani ya chuma au ndani ya bidhaa zozote kama unataka kuzalisha hapa lazima uangalie matumizi ya yale makapi. Inawezekana sisi tunataka kutengeneza kweli hicho kiwanda, lakini kuna makapi na bidhaa nyingine ambazo huenda tukawa hatuna matumizi nazo au soko la kuziuza au ubebaji wake zikishanyofolewa mle ndani ni kazi ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo suala la msingi ni kwamba wataalamu waangie, kama uamuzi unaweza kufanyika ili kwa mara ya kwanza baada ya miaka hamsini hiyo bidhaa tunayosema chuma iweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wasukuma mtu akija kununua mpunga kwao, unachouliza kitu cha kwanza ni bei ya mchele, ukijua bei ya mchele ndipo unajua kwamba niuze mchele au niuze mpunga; lakini utaangalia gharama zako, waste na nini, ndiyo utatoa bei ya mpunga. Kwa hiyo hata hili nafikiri wataalamu wajaribu kufanya vice versa waone kama mtu anataka chuma waangalie bei ya gharama zao na waangalie bei ya waste na nini ili waamue kama wanaweza kuuza ni vizuri Serikali ikauza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna hili tatizo la bidhaa ya mazao mbalimbali. Nimesikia wachangiaji, Waheshimiwa Wabunge hapa wameongea sana suala la mihogo kwenda kutafuta wateja China, kufanya nini; lakini mimi nilikuja hapa na wazo na kwenye Kamati tulijaribu kuliongea na kuliingiza. Lugha niliyotumia ilileta mtafaruku kidogo niliposema kwamba wananchi waruhusiwe kutengeneza gongo kutokana na mahindi, muhogo na mtama. Maana yangu, gongo ni kama kusema kitimoto kwenye nguruwe, lakini maana yangu ni spirit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gongo ni neno la mtaani kama vile kitimoto, lakini maana yake ni spirit. Pombe zote kali tunazokunywa hapa ni spirit. Hata tukiwauzia Wachina mahindi au muhogo, wakatengeneza spirit ile ile wataturudishia sisi. Kwa hiyo, sasa hivi sisi tunachokunywa ni spirit kutoka kwenye mahindi ya watu wa nje. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Sawa sawa.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna ubaya gani Serikali isiruhusu gongo, iruhusu spirit itengenezwe. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iruhusu spirit kutoka kwenye mazao ya chakula ili iweze kusaidia na kuinua bei ya mazao. Najua kuna wachangiaji wengi kwenye mtandao wanajaribu kusema kwamba bei ya vyakula itapanda, lakini leo hatuna njaa ya chakula, njaa yetu kubwa ni pesa. Maana yake vyakula vimebadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mchele, leo tuna competition kubwa sana ya chips. Tunalia sana mikoa inayozalisha mchele, maana yake watu wameanza kula viazi vitamu ambavyo ni chips. Na sisi watu wa Mwanza na Shinyanga hatuwezi kulalamika kwa kuwa watu wameanza kula chips, ni pamoja na sisi wenyewe; na bahati nzuri watoto wameipenda chips. Sasa sisi wenye mchele tutafanya nini? Ni lazima tutafute option nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri wataalam wetu wajaribu ku-review kidogo mawazo, itatusaidia sana. Maana yake elimu tunayotumia imeandikwa zaidi ya miaka 50 na dunia inakwenda haraka: Je, wataalam wanajaribu kweli ku- review mawazo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najaribu kumalizia kwa kuongea, suala hili limetusumbua sana hasa kwenye Kamati yetu ya Madini tulivyokuwa juzi kwenye kikao. Mheshimiwa Rais ame-invest pesa nyingi sana kwenye ndege zaidi ya shilingi trilioni moja. Ndege hizo tunatarajia ziende nje zikalete watalii na watalii watuletee dola. Hata hivyo, dola sisi hatui- charge tax, lakini dhahabu tunai-charge tax na dhahabu ni currency. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Ni fedha!

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dhahabu ni pesa na ni pesa ya kwanza kabla ya pesa hizi tunazozitumia za karatasi. Nafikiri kwa nyie wenzetu wasomi mnaelewa, pesa ya kwanza duniani ni dhahabu, lakini kwa nini tutumie gharama ya shilingi trilioni moja kufuata dola kwa Mchina Uchina? Tunakataa currency ya mtu ambaye hana viatu wala kitu chochote, hajaomba huduma ya Serikali, anatuletea dhahabu; na leo tunalia na Mheshimiwa Mpango, tuna deficit ya dola; lakini dola zipo mlangoni na watu walionazo hawana tatizo lolote. Tunataka tax ya nini? Mbona dola hatui-charge tax? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda na dola kwenye benki, unachoulizwa zaidi ni kwamba unazo nyingi tukuongeze bei? Mbona huyu wa dhahabu haambiwi kwamba unazo tukuongeze bei? Badala yake anaambiwa tutakukata. Ukimwambia utamkata, anakataa. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wataalam wetu wajaribu sana ku-review, maana yake elimu wanayotumia, hatukatai, lakini elimu isiwe kama Biblia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi hata Baba Mtakatifu anafanya marekebisho kwenye Kanisa Katoliki ili kusudi Kanisa lisiwe gumu na Walokole wasimalize wafuasi. Maana yake kwa ajili ya ugumu ule, Walokole wameendelea kuchukua wafuasi. Kwa hiyo, tunaomba na ndugu zetu; Mheshimiwa Mpango, jaribu kidogo kuchukua na elimu ya Mtaani ili ijaribu kutuinua kwenye uchumi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami niungane na Wabunge wenzangu walioshangia kwenye hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Suala hili la elimu naona kama ni suala kubwa kuliko hata suala la Katiba. Ukiangalia juzi TRA walitangaza nafasi 70 za kazi, waliojitokeza ni wanafunzi 40,000. Suala hili ni suala ambalo Wizara ya Elimu ilitakiwa isikitike na iogope sana na vyuo vikuu vilitakiwa visikitike na vishangae sana. Wewe una watu 40,000 wakapata kazi watu 50, hawa wengine wanakwenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu yetu hii tulirithi kutoka kwa wakoloni, kwa Waingereza haina pingamizi, wakimaliza watu laki tisa wakastaafu, Uingereza kwa mfano, watakaomaliza shule au university watakuwa milioni moja. Kwa hiyo laki tisa watapata kazi, hawa laki moja Serikali inaweza kuwatunza na kuwahifadhi. Lakini kwetu sisi wanaomaliza shule wanaweza kuwa milioni moja wanaopata kazi ni 50,000 kwa hiyo tukiendelea na utaratibu huu nadhani tunatengeneza bomu kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili naona kila mtu anaogopa kupasema lakini ukweli ni vizuri tukubaliane na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambao wao ndio watunga sera za elimu, tukubali iundwe Kamati au Tume ambayo itachunguza suala zima la elimu kwa Tanzania. Mheshimiwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, amejaribu kuliongea hili suala mara mbili, mara tatu, lakini naona kama watu hawalichukulii kwa uzito. Watu 40,000 ukachukua 50,000 kama wangekuwa Uwanja wa Taifa wakasema hawatoki mule uwanjani utakuwa na kazi ngumu sana ya kuwatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni vizuri watunga sera watutengenezee Sera mpya ya Elimu ambayo itawafundisha watoto wetu kutoka shuleni, darasa la kwanza wafundishwe shughuli zao za nyumbani; iwe biashara, kilimo, ufugaji na asilimia 50 ya maksi wapate kutoka huku, asilimia 50 wapate za darasani. Itatusaidia wakati mtu anakuja kumaliza sekondari au university hata unapomwambia aende akajitegemee kweli anayo sababu ya msingi na anafahamu atajitegemea nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kumwambia mtu aende akajitegemee, wewe umechukua pesa zake milioni 10 za university ukampa unayosema wewe ni degree, lakini kiukweli umempa karatasi. Umempa karatasi kwa sababu ni sawasawa na mtu amecheza DECI; hii degree hakuna mahali inapotambuliwa kokote, hata kama unaumwa huwezi kuiweka dhamana pharmacy, huwezi kuiweka dhamana benki. Sasa inawezekana kweli; mimi nimesomesha mtoto wangu, nimeuza mifugo yangu nimelipa milioni 10, wewe umenipa degree halafu wewe unaniacha mimi nikazunguke mtaani na ile degree na sidhani ukifika kwenye mji ulioathirika kama huo mimi mwenyewe ni muathirika wa degree, ninao watoto sita wana degree, kwa kweli inahuzunisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingekuwa bora watunga sera tukubaliane kwamba vyuo vikuu kabla havijatangaza nafasi za shule vikatafute ajira pia na vyenyewe, vieleze mishahara kwamba tumepata NBC shilingi laki nane mshahara, tumepata NSSF laki tano, sasa tunaanza kusajili lete milioni tano nitakupa degree kazi hii hapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, linaweza kuwa suala la kuchekesha, lakini hali ni mbaya sana kule mtaani; watu wanazo degree kila kona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini muda wa kusoma vilevile watunga sera wauangalie upya. Ni kweli nani alifanya research kwamba ubongo wa binadamu unahitaji kila mwaka darasa moja, kama yupo atuambie. Wakati huu nafasi za ajira hakuna, unachukuliwa mtoto wako miaka 17 unarudishiwa ana miaka 25, unaambiwa katafuteni kazi ya kujitegemea, mnajitegemeaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama watakubali watunga sera mwaka mmoja watu wasome madarasa matatu au manne ili watu wamalize shule mapema itatusaidia sana ili mtu akimaliza shule arudi huku tuje tuendelee na maisha kijana akiwa bado mdogo. Leo wanakaa naye muda wote wanakuja kukurudishia wewe miaka 25, huwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye familia zilizoathirika kwenye suala hili la elimu ukasema elimu ni ufunguo wa maisha, watakwambia hapana, elimu ya leo ya Tanzania ni kifungo cha maisha. Maana yake ni gereza ngumu sana; umefungwa wewe, amefungwa mtoto, amefungwa mama na pesa zimekwenda na umezeeka, wote mna vyeti viko ukutani na majoho ya siku ya graduation, cha kufanya hakuna, mnatazamana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina nia ya kubeza elimu lakini wakati huu uliopo ni lazima tufanye mabadiliko makubwa sana vinginevyo tunaziona nchi nyingi sana duniani sasa hivi zina matatizo makubwa kama haya. South Africa wanalo tatizo kwa sababu wote wamefuata elimu hii hii tu ya Mwingereza ambayo ni sukuma document basi, hakuna kitu kingine. Mwisho wa yote leo tuna shida kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana sana, kwa kuwa suala hili linaonekana limemtesa kila mtu, Mheshimiwa Waziri akubali kuunda Tume kama Mheshimiwa Rais Mstaafu Benjamini Mkapa alivyosema ili ijaribu kuchukuwa maoni kuhusu suala hili. Tume hiyo ijumuishe na wananchi wa kawaida siyo lazima wawe wasomi tu wawepo na watu wengine maana sasa hivi waathirika ni wengi sana sana, kiasi ambacho hali ni mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda kijijini kwenye majimbo ukiwauliza wananchi ni mtoto yupi mwenye faida hapa kijijini. Kama siyo uongo wanakwambia mtoto ambaye hajasoma ndiye mwenye faida kijijini. Anafuata wa darasa la saba, wa form four halafu wa degree. Wanasema wenye degree wanasema ni kama viazi vilivyoshindwa kuiva. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema hivyo kwa sababu hawezi kulima au kufanya kazi yoyote, anasubiri ajira na ajira hakuna. Kama zimetangazwa nafasi 50,000 walioomba ni 40,000 na hawa ndiyo wana email na internet, je, ambao hawana email na walioghairi ni wangapi. Je, watu hawa wapo wapi sasa hivi na wanafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu alifikirie sana suala hili. Najua watu wengi wanaogopa kulipasua. Nasikia Mheshimiwa Waziri anasema aboreshe elimu lakini unaboresha elimu ipi kama watu hawajapata kazi uliyozalisha? Bidhaa inaboreshwa pale ambapo bidhaa uliyopeleka sokoni wateja wamesema tunataka bidhaa aina fulani, ukisema unataka kuboresha elimu unaboresha ipi kama watu walio bora… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami naungana na Wabunge wenzangu kuchangia Muswada huu wa bajeti yetu ya 2019/2020. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais, Mawaziri, Naibu na Watendaji Wakuu wote wa Serikali kwa kazi kubwa sana wanazofanya na vile vile nawapa pole kwa kazi kubwa na mafanikio yanaelekea kuonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuiondoa elimu ndani ya maendeleo, lazima twende nayo. Kwa hiyo, nasimama sehemu ya elimu peke yake. Suala hili la ajira tusijaribu kuitupia Serikali lawama, ni vizuri tutafute ufumbuzi ambao unaweza ukatusaidia aidha kuipunguza kwa nusu au kuimaliza kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanzia chini kabisa. Utaratibu huu wa watoto wa shule kwenda asubuhi, kama hatuna nafasi za kazi, ni vizuri tumwombe Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Naibu wake yuko hapa, aufikirie upya hasa kwa watu ambao ni wakulima, wafugaji na wafanyabiashara ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wetu wanaamka saa 12.00 kwenda shuleni. Wakifika shuleni wanaanza kukimbia mchakamchaka. Baada ya mchakamchaka, saa 3.00 wanaingia darasani. Mpaka kuja kuanza masomo ni saa 4.00. Kwa nini watoto wasiende shuleni saa 5.00 wakiwa wamefanya kazi nyumbani ambapo tunatarajia kuja kuwarudisha huku wakimaliza University? Watakuwa wamefanya kazi nyumbani mpaka saa tano wataenda shuleni, watarudi kutoka shuleni saa 10.00 au saa 11.00.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli binadamu wote ni sawa, lakini Watanzania wote sio sawa, hilo ni lazima tukubaliane. Utaratibu huu wa kwenda asubuhi shuleni ni utaratibu wa Uingereza na nchi za Ulaya. Nchi za Ulaya bwana na bibi wanafanya kazi na hawana kazi nyingine pale nyumbani. Wanaondoka na watoto wao wanawaacha shule. Mume au mke anapowahi anampitia yule mtoto au watoto anarudi nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Ulaya kuna tishio la barafu. Barafu inaweza ikapiga London siku tatu, huwezi kurudi nyumbani au kutoka ndani. Kwa hiyo, kumwacha mtoto nyumbani au kumwacha anafanya kazi, hakuna kazi yoyote Ulaya ya kufanya, ni lazima uwapeleke shule. Sisi tunazo kazi za kufanya, kwa nini watoto wetu wasiende shuleni saa 5.00 mpaka saa 6.00 wakiwa wamefanya kazi huku?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tuna watoto wanaosoma shule za kutwa za msingi zaidi ya milioni nne mpaka tano. Wakifanya kazi masaa manne nyumbani wakazalisha kilo moja moja ya mahindi, mtama au mpunga, tutakuwa tumeinua uchumi wetu lakini watoto wetu watakuwa wamepata elimu ya kutosha; ili watakapomaliza University, tunapowalazimisha wajitegemee, hawatakuwa na tatizo lolote la kurudi kijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, ni suala hilo hilo la elimu. Wizara ya Elimu, mara kwa mara namsikia Mheshimiwa Waziri anapambana na watoto watoro, lakini kwa utafiti na maoni tunayoyaona hapa, watoro ndiyo watu waliofanikiwa kwenye maisha. Kwa nini sasa Wizara ya Elimu isianze mtaala wa watoro? Iwe na mtaala wa watoro na mtaala wa watu wazuri. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivyo? Leo hii tumeshuhudia watu watoro wakifanya maendeleo makubwa sana. Leo tuna wanamichezo na wanamuziki na bahati nzuri na humu Bungeni tuna zaidi ya Wabunge 50 ambao ni watoro lakini wana mafanikio makubwa sana. Kwa ridhaa yako kama utakubali nitaje hata kumi… (Kicheko)

WABUNGE FULANI: Wataje.

T A A R I F A

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Silanga.

MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa Mheshimiwa Kishimba yeye ni sehemu ya mtoro lakini alifanikiwa sana kuchenjua dhahabu pamoja na mwaka 1992 kuanzisha ununuzi wa pamba hapa nchini lakini alikuwa mtoro hakumaliza shule ya msingi. (Makofi/ Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa jirani unasemaje na taarifa hiyo?

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, yeah, naiunga mkono. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli maneno haya yanaweza kuwa kama ya utani lakini mimi nimekwenda darasani nimefika darasa la nne, nimeelewa kitu wanachofundisha huku kina faida maeneo fulani naenda kuanza shughuli zangu kwa nini mimi nakamatwa? Mimi nimeishia darasa la nne nikagundua ndani ya elimu kuna faida ya kitu fulani na kinaweza kupata faida muda huu, nikaenda kuanza procedure na kile kitu, kwa nini mzazi na mimi tukamatwe kurudisha shuleni tuendelee miaka 20 isiyo na faida? (Kicheko)

MBUNGE FULANI: Child labour.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu anayesema hapa ni child labour, je, old labour inasemaje? Maana utaratibu wote huu tunaohangaika ni wa Ulaya. Ulaya baada ya miaka 18 mtoto anakuwa mali ya Serikali na mzee baada ya miaka 60 unakuwa mali ya Serikali unatunzwa lakini sisi ni wewe na wanao sanasana university anachokunyan’ganya ni pesa na mifugo yako anakurudishia mtoto, inatupa wakati mgumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ubaya gani Wizara ya Elimu ikawa na mitaala ya watoro na Walimu wa wale watoro wawe ni wale watu waliotoroka shuleni ambao wameonesha mafanikio. Kweli mimi ni darasa la saba lakini Christopher Columbus aliyevumbua America safari yake ilikuwa kwenda India lakini akapotea kwa utoro akavumbua America. Mbona wote tunaenda kuomba pesa America nani anayewakataa Wamerikani kuwaita ni watoro. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la elimu ni lazima kabisa Wizara ya Elimu ifanye utafiti kwa vitu vingi sana. Leo hii VETA yetu kuna simu zaidi ya milioni 10 Watanzania wanazo lakini VETA haina mtaala wa kutengeneza simu. Leo tuna biashara mpya zimepatikana za madalali, hakuna Chuo cha Madalali lakini wako mtaani na wanaendesha shughuli zao wao VETA vitu walivyon’gan’gania haviko kwenye soko. Kwa hiyo, naomba sana sana Wizara ya Elimu waendelee kufanya mdahalo na wananchi ili tujaribu kujikwamua kwenye tatizo la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, leo hii usipopeleka mwanao shule unashtakiwa lakini mtoto akipata kazi wewe hakutumii hela huwezi kumshtaki. Tunaomba Wizara ya Elimu na Wizara ya Ustawi wa Jamii watuletee sheria hapa ili mzazi anaposomesha mtoto wake anapomuomba pesa au anapopiga simu watoto hawapokei wawajibike kisheria. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunahangaika kweli Majimboni, wazee wanakwenda TASAF mtoto yuko Dar es Salam ana maisha mazuri, kila siku unasikia ana birthday, mzazi aliyetumia ng’ombe nyingi sana kumsomesha mtoto anateseka. Haruhusiwi kwenda Polisi kulalamika na haruhusiwi kwenda Dawati la Jamii haiwezekani. Tunaomba Mheshimiwa Waziri lete huo Muswda, mbona wewe wanapofika form six unawakopesha, unawawekea na riba wanapopata kazi unawakata, mimi mzazi nina kosa gani kumdai mwanangu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini wazazi tujiandae kutoa radhi? Kwa nini mimi nijiandae kulalamika na kutoa radhi kwa nini Serikali isitusaidie, Mwanasheria Mkuu wa Serikali yuko hapa atusaidie, kwa nini tuwe tunalalamika, nitamlaani mwanangu, kwa nini nitoe radhi? Mwanangu nimemsomesha na nimemtunza kwa nini nijiandae kuja kutoa radhi badala ya Serikali kunisaidia sheria ndogo ili mtoto asipopokea simu, hakutoa pesa mimi niende Polisi ili apate Polisi Order anitumie pesa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa zoezi hili Serikali wameanza wao wenyewe ruhusu na wazazi ili mtu unaposomesha shule nijue na mimi kwamba nina invest kuliko sasa hivi naambiwa tu kwamba elimu unamwachia urithi wa kwako wewe, sasa urithi gani huo huyo amepata maendeleo yake wewe unabaki unazubaa kijijini, hauna chochote. Maneno haya tunayaongea kama mzaha lakini wazee kule vijijini wana shida nyingi sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Profesa Kishimba kwa mchango wako. Huyo ndiyo Profesa Kishimba nilimuita. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naungana na Wabunge wenzangu kuchangia Wizara hizi mbili za Kilimo, Uvuvi na Maliasili. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais, Mawaziri na Watumishi wote wa Wizara zote hizi. Naipongeza Wizara Kilimo hasa kwa suala kuondoa bei na indication price kwenye mazao yote itatusidia sana hasa kwenye mazao yetu ya pamba ambayo yalikuwa yana tusumbua sana wakati wa kutao bei na mara bei zinapoanguka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala hili la soko la mazao limeendelea kuwa tatizo kubwa sana. Kwa hiyo tunaomba Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda na Biashara zijaribu namna yoyote kuendelea kuwabana wenye viwanda hasa vya pombe na viwanda vingine waweze kutumia mali za Tanzania kwenye pombe au bidhaa ambazo sio za nje.

Mheshimiwa Spika, maana yangu ni kwamba kuna bia kama za balimi, kuna bia kama za eagle ambazo watumiaji ni watanzania ambazo watumiaji ni local. Vizuri wenye viwanda na Wizara Kilimo na Wizara ya Biashara ijaribu kuwabana ili kuwasidia wakulima wetu kupata bei za mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka jana nilikuja na suala la bangi, bahati nzuri nchi zingine mbili ukiondoa Uganda, Zambia na Malawi wameruhusu. Na vizuri mwaka 2015 Bunge lako hili lilipitisha nitaisoma sheria hiyo. Kifungu cha 12 cha Drug control and enforcement act. Cha 2015 kinaipa DCEA mamlaka ya kuruhusu ulimaji, usafirishaji wa bangi, mirungi, micocoa OPM kwa ajili yamatumizi ya tiba.

Mheshimiwa Spika, bei ya bangi duniani imepanda mara dufu na nchi zote zinazozunguka zimekwisha ruhusu. Wakati wa majumuisho tunaomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo… (Makofi)

SPIKA: Hii ni hoja muhimu sana naomba tuisikilize. (Makofi)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, naomba Waziri wa Kilimo kwa kuwa sheria hii ipo, aje atupe ufafanuzi kwamba watu wanaotaka kulima wamuone nani na imetungwa na Bunge hili mwaka 2015. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliopiga marufuku bangi ni wazungu miaka ya 40. Lakini wazungu wale wale wamegundua ndani ya bangi kuna dawa. Na sisi wenyewe tunaenda kwenye viwanda vya dawa. Je sisi tuki-import dawa yenye material ya bangi tutakuwa tuna-import toka wapi? Na tunatai-declare na namna gani?

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI: Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri Kairuki taarifa.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, naiona hoja ya Mheshimiwa Kishimba, lakini nipende kusema kwamba tayari hata sisi wizarani tumeshapata wawekezaji kama wawili wambao wameonyesha nia ya kuwekeza katika kilimo lakini pia kuchakata mafuta bangi kwa ajili ya matibabu. Tunaendelea kulifanyia kazi kama Serikali kwa sababu hakuna bado miongozo kifungu cha 12 kimeeleza kama itakubalika au laa! Ni hatua zipi na utaratibu gani uweze kufuata.

Kwa hiyo, nimuuombe Mheshimiwa Mbunge atuachie kama serikali na mamlaka zinazohusika tuendelee kulichaka na pindi litalopokuwa tayari basi majibu yatatolewa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kishimba taarifa hiyo.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, taarifa yake naiunga mkono, labda chakuomba kwa kuwa bei ya masoko ni bei ya ushindani ni vizuri Serikali ifanye uamuzi huo mapema zaidi.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma taarifa.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nilikuwa napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba kikawaida Bunge linapotunga sheria kinachofuata ni kanuni. Nilikuwa nafikiria Mheshimiwa Waziri angetuambia kanuni zipo tayari ili tuanze kulima maana bangi itaporomoka bei.

SPIKA: Mheshimiwa Kishimba endelea.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, sisi Tanzania kwa record kwa Afrika ni nchi tatu kwa kulima bangi ya magendo. Sasa kama wataruhusu na sheria kama ilivyo inaweza ikatusaidia sana kuongeza mapato na kuondoa magendo. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani yupo hapa kama anaweza kutoa msamaha hata kwa bangi iliyopo kwa miezi 6 kama msamaha anavyotoa wa silaha wananchi wakawasilisha bangi hizo polisi watu wakauziana polisi na TRA wakapata fedha na wanunuzi wakaja kununua hapa. Inaweza ikasaidia watu wetu wakapata pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vizuri wakati dunia inapobadilika lazima twende haraka sana, Uganda wamepewa hii AU zaidi ya dola ya milioni mia tano kwa ajili ya kilimo cha bangi wanatoa udongo toka Malaysia. Lakini sisi bahati nzuri wakulima wetu wana utalaamu wa kulima bangi muda mrefu. Kwa hiyo, kama serikali itapitisha na hiyo sheria kwa kuwa ipo, basi tumuombe Mheshimiwa Waziri wakati wote kama atapitisha iwe mapema kabla bei haijaporomoka. Ahsante sana nashukuru sana.

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa Spika.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge bado dakika za Mheshimiwa Kishima zipo pale. Lakini niwahakikishie this is not a joke anachochangia. Nilikuwa Canada majuzi hapa kwenye Mkutano wa Maspika wa Commonwealth duniani, ni big business in Canada, big, big business. (Makofi)

Kwa hiyo, anazungumza kitu cha msingi sana wala sio utani. Eeeh tena linaweza likawa zao moja kubwa kabisa la biashara linaloweza kuongoza kuliko mazao mengi tu, kabisa likafanya mapinduzi makubwa sana ya kipato. Kwa hiyo, anachokizungumza Mheshimiwa Kishimba hazungumzi bangi itumike vile ambavyo tunafahamu hapa nchini. Tunazungumzia habari ya kilimo moderated, monitored na utaratibu wote halafu wanapelekewa wanaohitaji kwa ajili ya kutengeneza madawa ya wanyama na binadamu. Malizia Mheshimiwa Kishimba dakika zako.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa hiyo tulikuwa tunaomba sana Wizara ya Kilimo wajaribu kulifikilia kama ulivyosema kwamba hii bangi sasa ni tiba. Kama ni tiba na sisi tunaagiza material kutoka nje na dawa kutoka nje ambazo zina bangi.

Ni vizuri sasa kutumia bangi yetu na huenda tukawa wazalishaji wazuri zaidi maana yake watu tayari wanao uzalishaji wa bangi. Na inaweza ikasaidia Wizara ya Afya kupunguza na kupunguza gharama za pesa tunazoagiza toka nje.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji amelisema vizuri kwamba na yeye lipo mezani, tunaomba wenzetu wa Zambia na Malawi wananchi wamelalamika kwamba baada ya kuwa imeruhusiwa, wameruhusu matajiri peke yake.

Tunaomba kama wataruhusu basi na wakulima wetu wadogo wadogo wapewe nafasi hizo ili na wao waweze kujipatia chance kwenye muda huu ambao zao hili litakuwa kwenye soko. Badala ya kuyapa makampuni makabwa peke yake ya nje ni vizuri na wakulima wadogo na watu wadogo wadogo wakaruhusiwa ili wote ku-enjoy bahati ambayo itatokea duniani. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii nami niungane na Wabunge wenzangu kuzipongeza Kamati zote zilizohusika; Kamati ya Afya, Kamati ya Elimu, Kamati ya UKIMWI na Madawa ya Kulevya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipo kwenye suala dogo tu la elimu. Asilimia 90 ya Watanzania wanaopeleka watoto wao shule, shida yao kubwa ni mtoto kumaliza shule na kupata ajira. Naona kwenye majumuisho yote, sioni mahali panapoongelewa suala ajira. Suala hili la ajira ni lazima tuendelee kulijadili kwa mapana makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwona Mheshimiwa Waziri anaendelea kufunga vyuo vingi ambavyo havikidhi mahitaji ya kielemu. Ushauri wangu, badala ya kuvifunga vyuo, Mheshimiwa Waziri alete Muswada humu Bungeni ili mtu akitaka kufungua chuo au kusajili wanafunzi ahakikishe asilimia 80 ya wanafunzi wamepata ajira ndiyo a-qualify kupata leseni ya chuo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, qualification ya chuo isije ikawa majengo kwa hali ilivyo sasa hivi. Mtu kama aweza kutoa ajira asilimia 80, yeye mwenye chuo ndio akatafute ajira ili hata kama mtu ana chuo chini ya mti, watu wetu wanapata ajira, apewe leseni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu sasa hivi ni kweli kuna utapeli mkubwa sana kwenye vyuo. Watu wetu wanalima, wanapika gongo, wanachimba madini kwenye matope, wanampatia mtu wa chuo kweli anawapa karatasi. Kama sheria itakuja hapa kwamba ili wewe uanzishe chuo u-confirm kwetu kwamba wanafunzi unaowachukua lazima wape kazi. Wasipopata kazi, ushitakiwe kwa kesi ya utapeli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, endapo Mheshimiwa Waziri ataleta huo Muswada Bungeni, unaweza ukatupunguzia mgogoro na watakuja watu wengi sana kufungua vyuo ili kusudi qualification ya chuo isije ikawa majengo. Hata kama mtu atasoma kwenye jengo zuri, kama hakupata kazi inamsaidia nini? Waheshimiwa akina Nelson Mandela na akina Mugabe wamesoma magerezani, lakini wamekuja kuwa viongozi leo na wote tunawatukuza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, hana sababu yoyote ya kugombana na wenye vyuo; alete Muswada Bungeni, tupitishe Muswada, mtu yeyote anayetaka kuanzisha chuo; Waganga wa Kienyeji wanafundishwa Uganga, watu wanaendelea vizuri na Waganga tunawaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaye humu Mheshimiwa Karamagi, Waziri wa Nishati, ni Mganga wa Mifupa. Alisoma chuo gani? Ni Mganga wa Mifupa! Kwa hiyo, nakuomba … (Kicheko)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Kalemani.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Karamagi. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Naamini ulimaanisha Mheshimiwa Kalemani, siyo?

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, Kalemani, yah, yah, ni Mheshimiwa Kalemani. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kalemani ni Mganga wa Mifupa na anatibu na anaponyesha, lakini hakusoma kwenye chuo chenye majengo, alisomeshwa kwenye Chuo cha Waganga wa Kienyeji na ni Mganga. (Makofi/Kicheko)

(Hapa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge waliongea bila mpangilio)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana wenzetu hawa wa mitaala ya shule; watu wanaikwepa VETA sasa hivi, naona Waheshimiwa Wabunge wengi humu ndani wanazungumzia suala la VETA, wananchi hawaitaki VETA kwa sababu VETA unaenda kujifunza kupaka rangi miaka mitatu, inawezakana kweli kupaka rangi miaka mitatu? Haiwezekani! (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani kujifunza kupaka rangi miaka mitatu. Mtu kama ameelewa kupaka rangi na soko halihitaji cheti, kwa nini siku nne asiondoke akaendelee na shughuli za zake? (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba Mheshimiwa Waziri afungue uwazi, watu wote watakubali. Kwa mfano, kutengeza simu; mtu aruhusiwe kutengeneza simu, akishafahamu siku nne, mruhusu aende akaendelee na shughuli zake. Maana soko haliulizi cheti. Hakuna mtu anaenda kutengenezewa simu kwa kuulizwa umesoma wapi na cheti kiko wapi? Unapeleka simu yako wanakutengenezea. Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu atusaidie sana ili kupunguza huu mgogoro. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la hospitali, tunaishukuru sana Serikali kwa hospitali, zahanati kila kitu kipo. Tatizo kubwa lililopo ni kwenye matibabu hasa X-Ray na vitu vingine. Ukienda benki kuuliza statement au kuuliza balance ya pesa, hawakuchaji gharama ya kompyuta, kwa sababu ile kompyuta ndiyo investment ya benki. Sasa inawezekanaje nikienda hospitali unanichaji gharama ya X-Ray? Kwa hiyo, X-Ray ni investment ya hospitali, maana inamsaidia Daktari kujua ugonjwa wangu, haiwezi kuwa package ya kunichaji mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotokea, wewe ukifika unaumwa mle ndani, hawa wana X-Ray karibu nane; kuna Ultrasound na nyingine. Unapelekwa zote sehemu kumi, halafu unaletewa bill unaambiwa ni shilingi 300,000/= halafu unaambiwa nenda kanywe maji mengi. Inawezekana kweli! Haiwezekani na hakuna mtu anaweza akambishia Daktari. Nani humu anaweza akambishia daktari? Haiwezekani!

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunamwomba Mheshimiwa Waziri wa Afya na Kamati yako, tunaomba mtengeneze mamlaka kama EWURA ambayo itadhibiti bei za dawa na bei za vipimo. Haiwezekani sisi tunadhibiti mbolea, tunadhibiti mafuta lakini hatuna mamlaka inayodhibiti bei ya vipimo na bei ya dawa. Haiwezekani! Maana yake sasa hivi ni tatizo kubwa kweli! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli jamaa zetu hapa walikuwa wanalalamika kuhusu suala la maiti; kuna matatizo makubwa sana. Mtu amefariki, acha ile issue ya bill, kwa sisi kama Waislamu, ukifika pale wanakwambia tumeshaihudumia maiti, tunakudai shilingi 300,000/=. Sasa unashangaa, sisi tunataka kuzika leo, wanakupa bill kwamba wameshaihudumia maiti. Sasa wewe hujui umehudumiwa nini? Kwa kweli Mheshimiwa Waziri wa Afya, tunaomba sana sana, hasa sisi Wabunge ni tatizo kubwa sana. Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Afya ajaribu sana kufikiria suala hilo. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho kabisa ni usajili wa Zahanati. Medical Assistant akitaka kusajili leo Zahanati, shida anayopata matokeo yake wanazifunga. Daktari aliyestaafu akitaka kusajili hospitali, anashindwa; lakini Mganga wa Kienyeji anasajili ndani ya dakika kumi na anaruhusiwa kulaza wagonjwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa inaingiaje akilini? Wote humu mnafahamu, mmesoma na Madaktari wamo, kweli Mganga wa Kienyeji anasajili dakika kumi, Medical Assistant au daktari bingwa mstaafu hawezi! Anapata shida ngumu sana na wote wanazifunga. Leo watu wa mionzi wanazunguka wanaendelea kufunga Zahanati, lakini Waganga wa Kienyeji wanaendelea kulaza wagonjwa. Itawezekanaje? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli ni kitu ambacho kweli kinaingia akilini! Tunaomba sana Kamati ya Mheshimiwa Serukamba, afikirie kabisa shida ya wananchi wanayoipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo, nashukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Kilimo. Kwanza nawapongeza Manaibu Waziri na Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa wanayofanya kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, leo suala langu ni gumu kidogo ingawaje kabla sijaanza watu wanaanza kucheka. Mimi nakuja na suala la bangi, nchi nne za Afrika sasa hivi zimeruhusu kilimo cha bangi kwa ajili ya matumizi ya dawa za binadamu. Ni vizuri wakati wowote wakati dunia inapopata nafasi…

SPIKA: Hebu Waheshimiwa Wabunge tusikilizane, yanapoongelewa mambo ya maana na muhimu tunasikiliza, Katibu weka vizuri dakika zako hebu anza vizuri, Mheshimiwa Kishimba endelea.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ni vizuri sana wakati dunia inapopata kitu kipya na sisi Watanzania kuwa wa kwanza kuwahi kama wenzetu wanavyowahi. Ninavyoongea gazeti la Mwananchi la tarehe 18 mwezi wa Tano Jumamosi, nchi ya Uganda imekwisharuhusu kulima bangi kwa ajili ya dawa za binadamu. Dawa nyingi za maumivu hasa za kansa Mheshimiwa Waziri wa Afya, Naibu Waziri wa Afya Mheshimiwa Ndugulile anafahamu vizuri kwamba nyingi kwa asilimia 80 zinatokana na bangi.

Mheshimiwa Spika, nashangaa kwa nini wataalam wetu wa TFDA wangekuwa wameshachukua sampuli muda mrefu wakati wanaziangalia kwenye maabara, wangetujulisha kwamba ndani ya hizi dawa kuna bangi na wangemuuliza supplier hii bangi unapata wapi. Maana yake sisi wenyewe tunayo bangi na ukiangalia vizuri bangi tunayoona kila siku inakamatwa kukatwa ukweli bangi hiyo siyo kwa ajili ya kuvuta, bangi hiyo imekuwa ikienda kwenye dawa za binadamu. Ushahidi ninao Lesotho na Zimbabwe wameruhusu na mimi nimefika kwenye kiwanda cha Zimbabwe ambacho kinatengeneza dawa za binadamu kwa kutumia material ya bangi.

Mheshimiwa Spika, gunia moja la bangi leo Tanzania ni shilingi milioni nne mpaka milioni nne laki tano, lakini Lesotho na Zimbabwe ni dola elfu saba, karibu milioni ishirini na bangi yote hii ya Tanzania yote inakwenda kwenye madawa ya binadamu ambayo sisi tunaletewa kuja kutumia kwenye hospitali zetu. Sasa kuna ubaya gani Serikali ikaanza kutoa permit au vibali watu kwenye maeneo mbalimbali na kuhalalisha watu waanze kulima bangi hiyo ili tuweze kupata faida na kuondoa mgogoro mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siwezi kuungana na Mheshimiwa Musukuma kwenye suala la kuvuta, suala la kuvuta sheria iendelee palepale kwamba watu hawaruhusiwi ,lakini kwa kuwa sasa ni halali kwa ajili ya madawa ya matumizi ya dawa za binadamu, tuna sababu gani ya msingi sisi kutowahi hilo soko? Hata kama tutakataa leo, baada ya miaka minne wakati bei itakuwa imeanguka hata tukiruhusu haitatusaidia. Ni vizuri Waziri wa Kilimo awasiliane na Waziri wa Afya waone namna gani watafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ilivyo bangi ni zao ambalo kwanza haliliwi na wadudu, hakuna wadudu wanaokula bangi na eka moja ya bangi unapata gunia sita. Kama ni gunia sita kwa bei ya milioni 20, ni milioni 120 lakini leo wananchi wetu wanauza milioni nne na ndiyo zao peke yake Tanzania kwa leo ambalo mkulima akiwa amepewa advance, Mheshimiwa Heche naona ametoka. Kwa hiyo badala ya kuendelea na mgogoro huu tunaomba Wizara ya Kilimo wafikirie contract farming ya bangi ambayo sasa inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi ya Canada imeruhusu, yenyewe imeruhusu kuvuta, lakini Canada ni miongoni mwa nchi saba tajiri na Mheshimiwa Waziri wa Fedha nafikiri anatarajia kuomba pesa huko akipewa pesa za bangi atakataa na atazijuaje kwamba hizi ni za bangi. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nafikiri ni vizuri sana, tumeona tumepoteza vitu vingi sana kwa ajili ya kuchelewa. Tulikuwa hapa meno yetu ya tembo yanakwenda Burundi kwa miaka 30, mpaka mwishowe biashara ya meno ya tembo imekwisha. Tumeshuhudia dhahabu zetu zikienda tunachelewa sana sana kufikiri, juzi hapa kwenye Uwanja wa Ndege wa Entebbe tarehe 11 Machi zimekamatwa tani saba za dhahabu. Ukiangalia tani saba za dhahabu Uganda haina dhahabu, dhahabu hizo zimetoka Tanzania, lakini namna hii hii tunachelewa baadaye dunia inabadilika si tunaendelea kulima matikiti maji. Tunaomba na uzuri kama Waziri wa Kilimo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali yuko hapa kama watapitisha hili na Wabunge nafikiri watakuwa watu wa kwanza kabisa kujisajili na hali yetu kama unavyoijua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, yeah, ahsante sana; na mimi niungane na Wabunge wenzangu kuwapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na Watendaji wote Idara ya Madini kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, mimi ninayo shida kubwa sana kwenye Mgodi wangu wa Buzwagi. Mgodi huu unaenda kufungwa au kufukiwa; mgodi huu juzi kwenye ziara ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Naibu Waziri Nyongo alikuwepo na Mawaziri wengine; Meneja wa mgodi alituhalifu kwamba mgodi ule bado una balance ya dhahabu ounce audhi milioni moja, ni sawa sawa na kilo 31 za dhahabu. Anachodai Meneja wa mgodi ni kwamba gharama zao za uzalishaji ni kubwa.

Mheshimiwa Spika, kilo 31 ni sawa sawa na dola bilioni 1,200,000 ambazo ni sawa na trilioni 28. Kinachonishangaza hapa; ni kweli tukubali kwenda kufukia mgodi wenye dhahabu ya trilioni 28 ilhali sisi tunauwezo wa kufunga mto Rufiji tukapata umeme?

Mheshimiwa Spika, lawama lazima tuitupe tu kwa wataalamu ukweli ni wavivu kwa kufikiri, hauwezi ukaletewa ripoti na mtu mmoja mwenye mgodi akafukia mgodi wako wenye thamani ya trilioni 28 na wewe unashida ya kujenga Standard Gouge wewe uko tayari kuziba mto Rufiji, haiwezekani, ni kitu ambacho kinauzunisha sana. Serikali kwenye Sheria yetu mpya ana asilima 16 mle ndani ina maana na Serikali atapoteza na kodi tutapoteza. Lakini alichosema Meneja wa mgodi ni kwamba gharama zao ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi niombe kwa Mheshimiwa Waziri au wewe utusaidie. Iundwe tume ndogo iende ikaangalie gharama za uzalishaji za mgodi huo; zile ambazo zinaweza kuondolewa ziondolewe. Lakini Serikali upande wake pia ifikirie; maana TANESCO anapata bilioni mbili kwa mwezi, TRA anapata na yeye zaidi bilioni 20 Idara ya Maji tunapata zaidi ya bilioni nne. Hawa kama wanaweza na wao kupunguza tariffs zao wapunguze maana kama mgodi utafungwa hata hizi tariffs zao hazitafanya kazi popote. Ikiwezekana wapunguze ili tuunusuru mgodi huu.

Mheshimiwa Waziri tumekuwa tukiongea mara kwa mara lakini bado mimi nawasiwasi kwamba wataalam wetu ni wavivu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili ni suala zima la madini. Utajiri wa Warabu ni mafuta, na Warabu wamepata utajiri wa mafuta pale bei ya mafuta inapopanda. Sisi tunayo dhahabu, wahasibu wetu wanachanganya kati ya hesabu ya kiwanda na hesabu mining. Dhahabu haipandi kwa ajili ya gharama ya uzalishaji, dhahabu inapanda kwa hali inayoendelea duniani. Kama kuna hofu au tatizo lolote dhahabu itapanda.

Mheshimiwa Spika, sasa nachojaribu kujiuliza hapa; na nafikiri Mheshimiwa Waziri itabidi hapa nishike shilingi ili tupate ufumbuzi. Bei ya dhahabu mwaka 2008 ilikuwa gram moja ni dola 40, ambapo ni kama ounce moja dola 800; leo ni dola 60; lakini gharama za uzalishaji hazikupanda, maana raw material ya dhahabu ni mawe ambayo ni asilimia 70, kilichoongezeka hapa hakikuongezeka kwa sababu ya gharama ya uzalishaji, kimeongezeka kwa sababu ya demand duniani tofauti na kiwanda. Serikali ya Tanzania kama wahasibu au wataalam wetu watakubali, tunakuwa na utajiri mkubwa sana pale bei ya dhahabu inapopanda; ile pesa si pesa ya mweye mgodi wala mwenye mgodi hawezi kuidai, kwa sababu hata dhahabu isipopanda yeye anaendelea na uzalishaji na faida anapata. Warabu wametajirika ni pale bei ya mafuta inapopanda duniani, ile tofauti inatakiwa kuwa yote ni mali ya Serikali siyo mali ya mwenye mgodi . Maana yake hiki ni reserve ya ile nchi ndiyo faida yake iko hapo; wataalam naona bado linawapa shida sana suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya muda naomba niungane kwenye suala moja na Mheshimiwa Heche. Mheshimiwa Heche amesema, ni kweli ile migodi haijawahi kutulipa service levy yetu mpaka sasa hivi. Service levy hiyo anayoisema inahitaji ufafanuzi kidogo; ni kwamba hizi mining zote zilizoko Tanzania zina bima tatu, zina bima ndani ya dhahabu inapokaa, zina bima ya mgodi mzima, zina bima zinapotaka kwenda kukopa benki maana yake zote zimekopa benki lazima ziweke bima; kwa hiyo zina bima tatu. Bima hizi ni zimelipiwa Ulaya kweli, lakini kwenye tariff ya TRA wame-deduct kama cost. Kwa hiyo zile pesa tunatakiwa sisi tulipwe service levy yetu ambayo ni zero point three.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo hii pesa siyo ya mgodi ni ya yule mtu wa insuarance ambaye yupo; ni watu wa mgodi tu kutuambia kwamba ni huyu hapa na invoice tumpelekee, si mali ya mgodi hata siku moja na hawa watu wa insurance hawajawahi kujulishwa mimi ninavyojua; na watakataa kwa sababu hawajawahi kulipa kitu chochote wana benefit wao. Ingetusaidia sana, kama alivyosema Mheshimiwa Heche na Mheshimiwa Musukuma kwamba ni vizuri watusaidie.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami niungane na Wabunge wenzangu kuchangia Mpango huu wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Spika, nimeusoma Mpango huu vizuri sana lakini kuna mahali ambapo sipaoni pametiliwa umuhimu napo ni sehemu ya afya. Suala hili la afya kwa sasa sisi Majimboni ndiyo suala ambalo ni gumu sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Mwalimu Nyerere mpaka mwaka 1985 ilikuwa inatoa matibabu bure kwa raia wote wa Tanzania. Wakati huo tunafahamu vizuri labda tu kwa vijana, Serikali ilikuwa imefilisika baada ya vita vya Uganda lakini Serikali ilikuwa inatoa matibabu bure. Leo nikiangalia kwenye Mpango hakuna mahala ambapo panaelezea namna gani wananchi wetu wapatapa matibabu. Mheshimiwa Sunga ameeleza vizuri watu wetu kweli ni maskini na bei za matibabu na dawa mwananchi wa kawaida wa Tanzania hawezi. Namuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha afikirie kama anaweza kuongeza bei kidogo au shilingi 30/40 kwenye mafuta ili wananchi wetu tuwapatie matibabu bure. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nalisema hili kwa sababu leo tunakusanya shilingi trilioni 2 na waliotuchangia hizi shilingi trilioni 2 ndiyo hawa, ni sahihi kweli mwananchi akienda hospitali akiwa hana pesa hakuna kitu chochote anaweza kufanya matokeo yake anaenda kukabiliana na kifo. Ni sahihi sisi Wabunge wote tunatoka Majimbo ambayo yana matatizo makubwa sana, hakuna Mbunge ambaye ametumwa nyama au sukari na wapiga kura wake labda Mheshimiwa Gwajima Mchungaji Kawe kwa kuwa Jimbo lake ni zuri kidogo lakini sisi kwenye Majimbo yetu hali ya umaskini wa wananchi wetu ni mbaya. Kwa kuwa wananchi hawa hawana tatizo la nyama wala sukari, wanaipita nyama hapo wanaenda kununua mchicha bila hata malalamishi tatizo lao ni dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri ugonjwa ni kitu ambacho mtu hawezi akajisingizia. Sidhani kama hofu ya Serikali ya kutoa matibabu kuwa bure kama ina sababu ya msingi. Kwa sababu sidhani kuna nchi duniani ambayo iliwahi kutibu watu wake bure ikafilisika sidhani, haiwezi kufilisika. Duniani nchi zinafilisika kwa vitu viwili; ni vita na ujenzi, hakuna kitu kingine. Kwa mapato tuliyonayo, tunaomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha afikirie ili tukawatendee haki wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hili tatizo la bima Mheshimiwa Waziri wa Afya yuko hapa, bima ni sawasawa na kamari. Tunaona Polisi kwa wachezesha kamari endapo mchezesha kamari ameliwa, akiwa hana pesa polisi wanakuja, vipi mtu aliye na bima anapokwenda hospitali anapoambiwa dawa hakuna kwa nini Mheshimiwa Simbachawene asipunguze traffic barabarani atuhamishie baadhi ya polisi hospitalini ili mgonjwa anapoambiwa na bima hakuna dawa aende akaripoti polisi. Kwa sababu traffic anahangaika na mtu ambaye hakufunga mkanda ana Landcruiser ambaye akimuona traffic anafunga akitoka anafungua lakini huyo ndiyo anakimbizana naye. Mheshimiwa Simbachawene tuhamishie baadhi ya traffic wawe hospitalini ili mtu akikosa dawa aende pale polisi ili anusuru uhai wake. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hapo ndipo panapohitaji usalama kabisa huku kwingine kote tunasumbuka. Usalama unahitajika pale mtu anapokuwa anaumwa, aende mtu polisi kawaida kama wanavyotetewa wacheza kamari itatusaidia. Sasa hivi simu zote tunazopokea Wabunge nusu ni kwa ajili ya dawa na matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuwaombe pia wenzetu wa Wizara ya Afya, kwa nini hakuna regulatory kwenye hizi dawa na matibabu. Tuna EWURA kwenye maeneo ya mafuta, tuna TFDA na TBS, kwa nini kwenye dawa pana kigugumizi na wakati dawa ndiyo kitu cha muhimu na cha mwisho kabisa kwenye maisha ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, leo tumeshuhudia watu wana- charge dawa mpaka shilingi milioni 5, unaposema milioni 5 kwa mtu wa kawaida anazipata wapi pesa hizo. Vilevile tunaona sasa hivi ukiwa na bima ghafla wanakwambia tumeondoa hiki, wao ndiyo walipokea pesa, halafu wao tena katikati ndiyo walioamua kwamba ugonjwa huu tumeshauondoa na wewe umeugua na hauna kitu chochote, nafikiri hapo Mpango uangalie vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala hili la matibabu nafikiri hata mimi mwenyewe ningekuwa na maisha ya chini kule kijijini kwa hali iliyoko leo ni kitu kinahuzunisha sanasana. Tuwaombe Wizara ya Afya na yeye mwenyewe Mheshimiwa Waziri wa Fedha basi aruhusu hata bili za maji au bili za umeme ziwe dhamana ili mimi kama naumwa niende na bili yangu ya maji au umeme baada ya kupata ile hesabu ya hospitali wanigawanyie mle kidogo kidogo niwe nalipa pamoja na bili ya maji au umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naliongea suala hili kwa mapana kwa sababu hili suala linatusumbua sana. Unakuta mtu amepata matatizo unaambiwa kwamba huyu hana bondi ya pesa, hatuwezi kumtibu mpaka upate 300,000 za kuweka dhamana, je, huyo mtu anayesababisha kifo hiki kwa ajili ya pesa yeye siyo mhalifu kama wahalifu wengine? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna ubaya gani Serikali ikaweka utaratibu wa kukopesha wagonjwa kama inaona vigumu? Makampuni ya simu leo yanakopesha bila hata kumuona mtu mpaka shilingi laki tatu, Serikali yetu inaona ubaya gani kumkopesha mgonjwa matibabu? Atalipa tu maana tuna vitambulisho watu wote wanajulikana akopeshwe na baada ya mwaka kama itaona madeni yamekuwa hivi Serikali inaweza ikawafutia watu wake. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hawa ndiyo wapiga kura wetu, haya mambo yote tunaongea kiingereza sijui nini, mimi naona shida kubwa. Kwa kuwa suala la elimu limeanza kujadiliwa, suala ambalo limebaki na mgogoro ni suala la afya. Tunaomba sana kwenye Mpango huu Mheshimiwa Waziri alifikirie sana. Tumeweka shilingi 50 kwa ajili ya maji tumeweka Sh.50 kwa ajili ya REA, afikirie kama anaweza kuweka hata Sh.30 kwa ajili ya afya. Wataalamu wa uchumi wanasema vitu au maisha yatapanda ni uongo. Bei ya nauli ya daladala leo ina miaka mitano haijawahi kupanda pamoja na bei ya mafuta kupanda, hata nauli za mabasi hazijawahi kupata, hata mafuta yakishuka hatuoni impact yoyote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba wenzetu wataalamu wa uchumi wasije wakalivuruga wakasema sijui maisha yatapanda, maisha yapi, maisha ya Tanzania …

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, mnaona Maseneta wanavyo argue point, amekuja na issue yake leo ya afya na bima ya afya, dakika zake zote anazitumbukiza pale. Endelea Mheshimiwa. (Makofi)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni kweli wataalamu wetu wa uchumi wasije wakaleta yale matarakimu yao ya kusema ooh maisha yatapanda, uchumi wa Amerika ukiongeza bei ya mafuta ndiyo unapanda uchumi wa Tanzania hauna hata mahusiano. Leo vijijini hata mafuta ya taa hakuna kuna solar kila kona, kwa hiyo, mtu asilete tena maneno ya uongo, hakuna. Hata kama mafuta ya taa yakipanda kule kijijini kibaba huwa hakibadiliki huwa kina bei ileile tu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha alifikirie kwani tutakuwa tumewatendea haki sana wananchi. Kweli tumejenga zahanati kila mahala lakini wananchi wanahitaji zahanati bila dawa? Maana kama mwananchi haponi, haoni thamani hata ya ile zahanati.

Mheshimiwa Spika, ni hofu bure tu, leo tunakopesha wanafunzi zaidi ya shilingi bilioni 600, kweli tunakataa kumkopesha mtu uhai? Ni suala ambalo Mheshimiwa Waziri wa Fedha anatakiwa alifikirie kwa mapana kwenye Mpango wake. Hii itatusaidia sana na tutakwenda kule vijijini tukiwa kweli tuko huru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Majimbo yetu yale ya vijijini hawana shida ya nyama wala sukari. Sisi kwetu kijijini ukinywa chai wanakuuliza leo unakunywa chai unaumwa? Hawana tatizo, ni haya ya mjini ndiyo yenye matatizo lakini sisi hatuna tatizo la sukari hata wanashangaa tunapolalamikia sukari. Kwa hiyo, tunaomba Waziri wa Fedha atufikirie sana. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango huo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami naungana na Wabunge wenzangu kuchangia kwenye bajeti hii ya 2021/2022. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Baraza zima la Mawaziri pamoja na Kamati ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naishukuru sana Serikali kwenye suala hili la barabara baada ya kukubaliana na kilio cha Wabunge na kuweza kutenga pesa hasa upande wa TARURA. Nashukuru sana kwa sababu kama kilio cha Wabunge wote kilivyokuwa, ilikuwa ni tatizo kubwa sana kwenye maeneo yetu, nami mwenyewe kwenye Jimbo langu la Kahama nilikuwa mwathirika mkubwa sana wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye barabara naomba kushauri kidogo kwamba zamani mpaka miaka ya 1990 barabara zilikuwa na mtu anaitwa Road Surveyor ambaye alikuwa anaamka asubuhi akiwa na baiskeli; mmoja anakwenda upande mmoja kilometa tano, mwingine anakwenda na baiskeli kilometa tano akiwa amebeba koleo au jembe akiangalia zile sehemu ambazo barabara imeumia. Hii ilisaidia sana barabara zile kuendelea kutibiwa yale maeneo ambayo madogo madogo yanaoonesha ubovu, lakini baadaye watu hawa waliondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wenzetu wa TARURA, kama wanaweza kuwarudisha tena. Maana yake kwa sasa hivi kwenye maeneo yetu TARURA inakuwa na wafanyakazi wawili au watatu. Kwa wingi wa barabara, haiwezi kuzi-repair zile barabara mpaka mwakani. Kama unaweza kuwarudisha watu hao na leo tuna pikipiki, inaweza ikatusaidia sana kuliko kusubiri mpaka barabara zote zimeharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wetu ni kama tembo aliyebebwa na sisimizi, lakini tembo huyu huwa hafahamu kama amebebwa na sisimizi. Mara nyingi akipata shida kidogo huwa anapenda sisimizi watoke. Nasema hili nikiangalia hili suala la machinga. Sisi ambao tunatoka maeneo ambayo miji yetu haina ajira rasmi; kwenye Jimbo langu watu walioajiriwa na mishahara kabisa katika watu 500,000 hawafiki watu 5,000; na wenye mshahara ambao unaweza kutosha kutoka tarehe 1 mpaka 30, hawafiki 200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali inavyoendelea, Mheshimiwa Waziri inaonekana kama kuna mchaka mchaka dhidi ya machinga au wafanyabiashara wadogo wadogo kuja kuondolewa kwenye maeneo yao. Watu hawa tumekuwa nao zaidi ya miaka mitano, wametusaidia sana kwenye shughuli za kibiashara na wame-stable na wamepata ajira. Leo kama tutaona kwamba tuwatoe, linanipa shaka sana kwa sababu watu hawa wamesaidia sana maeneo mengi hasa kwenye shughuli za wakulima. Bidhaa wanazouza ukiacha zile za nje ni bidhaa za wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo viazi ulaya kwa wenzetu wa Kusini wameongeza ukulima mara tano zaidi lakini aliyesababisha viazi ulaya viende ni Mama Ntilie. Kwa sababu, leo huwezi kuipika chipsi nyumbani kwa sababu ukipika chipsi unahitaji zaidi ya lita mbili za mafuta, lakini mama ntilie na machinga wameendelea kupika chipsi hizo na kusababisha ulaji mkubwa sana wa viasi. Sasa sijui wenzetu wateule nini hasa kinachowabuguzi, maana yake leo mahindi wanayochoma ni mahindi ya wakulima, ina maana wamemsaidia mkulima na wao pia wamepata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wanauza miwa wanaikatakata wanaikamu miwa wanawasaidia wakulima wetu lakini na wao wanapata ajira. Nafikiri wachumi wetu wajaribu kwenda kwa data ndani zaidi, leo hii ukiangalia uuzaji wa kuku wa kizungu, waliosababisha ulaji wa kuku leo, siyo matajiri wala siyo watu wa hali ya juu, walio sababisha ni watu wa hali ya chini ambao mpaka wamewezesha watu kula utumbo wa kuku. Kwa sababu, leo wanaweza kumkatakata kuku mpaka shilingi 400, 500 kwa hiyo wamepeleka biashara hiyo na wamefanya nyie mnachosema kitaalamu wame add value nafikiri hawa ndiyo walio add value kuliko mtu yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea Serikali ikawape motisha lakini kama Serikali inang’ang’ana kwenda kuwatoa au kuwakataa na vijana wetu waliomaliza shule wote tunategemea waende kwenye kazi ya machinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye majimbo kama ya kwetu ambayo yameathirika sana na shughuli za migodini, ukiondoa wale wajane ambao wako kwenye Biblia na Quran, sasa hivi tuna wajane ambao wametelekezwa na wanaume na wana watoto kuanzia wanne mpaka watano mpaka saba, shughuli zao hawa wakinamama ni shughuli hizo hizo ndogo ndogo. Serikali yetu haina utaratibu wowote wa kumsaidia mjane, haina utaratibu wowote wa kumsaidia mama aliyetelekezwa na ana watoto atafanya nini unapomtangazia kiama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni rahisi sana mtu ambaye anamaisha mazuri kutamka, kwamba machinga wanaleta uchafu, nirahisi sana lakini machinga wamekwenda Oyster Bay wanatamuuzia nani? Hakuna machingia ambaye yuko Oyster Bay, hakuna mashinga ambaye anakwenda Masaki, kama wako Kariakoo sisi wenye hali nzuri ndiyo tumewafuata, tumeenda kutafuta nini kule kariakoo? Maana sisi tuna maduka yetu kule Oyster Bay yapo, sisi tunaenda kutafuta nini Je, tunaripoti yoyote yenye lawama zidi ya wenye duka na machinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kama sisi Kanda ya Ziwa hatuna ugomvi wa Wafugaji na Wakulima kwa sababu sisi tunazo ng’ombe zaidi ya miaka 200, lakini ugomvi uko kule Morogoro ambako wafugaji wameenda mara ya kwanza lakini machinga, hawajawa na ugomvi wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kinanipa kigugumizi ni nani hasa ambaye anawaza kwamba hawa watu hawafai. Baada ya uhuru tulikuwa na wahindi na wa-Asia na waswahili kwenye miji yetu, lakini mwaka 1980 baada ya kuvunjika ujamaa na viwanda collapse watu walibaki kule mjini, hawa wamezaliwa kule mjini baada sehemu hiyo imevutia, tena watu wameenda kukaa kule, hii ni kabila mpya imeonekana mjini, hawa watu hawawezi kulima, hawawezi kufuga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, tunataka waende wapi hasa, labda Serikali wakati wa kuhitimisha watupe jibu kwamba watu hawa wanatakiwa kwenda wapi? Hawawezi kulima, hawajawai kulima, wamezaliwa mjini hata kabila zao ukiwauliza wanasema kwetu Mwanza, kwetu Moshi lakini hajawai kufika Mwanza utawafanya nini? Nafikiri wateule wetu wajaribu sana kuwa wabunifu, watu hawa ni resources nzuri sana ya uchumi, nzuri sana wamefanya mabadiliko makubwa mno ya uchumi ila uwezi kuyaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye watu wa Mpesa sehemu zinazoongoza kwa kutuma Mpesa ni maeneo ya machinga peke yake ndiyo wanaongoza kwa kufanya biashara, hizi biashara bidhaa zote wanazouza, si Serikali amepata kodi. Lakini wao wanamlazimisha mtu kila mtu anatembea wanamlazimisha ina maana kazi wanayofanya ni kazi ngumu sana, sasa ni ajabu kama sisi tunaenda kungangana kuwatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, machinga ndiyo chuo kabisa original cha kutoa wafanyabiashara leo Watanzania, je, hii ya kwenu CBE imewahi kutoa mfanyabiashara yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ina maana tunakwenda kufunga chuo ambacho kinatoa watu original, tunaenda kufungua vyuo ambavyo havitoi wafanyabiashara tunaomba sana wenzetu hasa Mheshimiwa Waziri alifikirie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Muswada huu wa Bajeti ya mwaka 2022/2023. Pia mimi nam- support, namuunga mkono Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa sana aliyofanya, hasa hii juzi kwa hizi fedha shilingi trilioni moja, ukilinganisha na wakati huu wa Corona ambapo hali ya dunia kiuchumi siyo nzuri. Namshukuru sana na imetufikia kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kwa malalamiko makubwa hasa kwa upande wangu wa Jimbo la Kahama Mjini. Nimekuwa nikipata zawadi, heshima kubwa, nimekuwa wa kwanza kwenye mapato, kwenye makusanyo na kwenye kila kitu. Hata hivyo, ninavyoongea, barabara zangu za mjini ni mbaya sana. Haiwezekani mtu anayeongoza kwa mapato halafu unamnyima fedha ya barabara. Atapataje hizo fedha bila barabara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata sasa hivi, zile shilingi milioni 500 za Mheshimiwa Rais bado sijapata. Ninavyoongea nina shilingi milioni 18 peke yake. Sasa itawezekana mnanipa mimi zawadi na matunzo. Afadhali mtoe zile zawadi za ushindi, mnipe fedha za barabara. Baadaye nikiwa salama, mrudishe yale matunzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ulipita juzi Kahama ukiwa unaenda Chato. Kweli ukiwa barabarani pale unaona mji unang’aa, lakini kule ndani hali ni mbaya sana. Mapato ya Serikali yanayokuja yanatoka maeneo yale. Kwa hiyo, tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, atupatie hizo fedha ili wananchi hawa wakati huu msimu wa mvua unapoanza waweze kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo umeliongea, nami nilikuwa nakuja huko huko. Labda tu sasa kwa wachumi wetu tuone kama wanaweza kufanya namna. Maana yake wote tunaziona kero. Ujenzi unaoendelea kwa zahanati, hospitali; madarasa hatuna shida sana. Unaangalia, kweli vijiji vyetu au kata zetu hazikukatwa kama madarasa. Wananchi walikuwa wanakaa maeneo yale, lakini unapotamka kijiji ukasema utaweka zahanati kila kijiji au Kituo cha Afya kila Kata, unatumia uwiano gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati zile ni kubwa, Vituo vya Afya kwa michoro ile, inatugharimu kweli shilingi 400/= mpaka shilingi 500/=. Mahudhurio ya wagonjwa ni wagonjwa 20 au 18 kwa siku. Kwa nini Serikali wasijenge jengo dogo la shilingi milioni 30, ile shilingi milioni 370 ikawekwa benki kwenye fixed account, fedha itakayopatikana iwatibu wagonjwa bure iwape mpaka uji? Maana yake wagonjwa hawafuati jengo, wagonjwa wanachofuata ni dawa na huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vijiji kwa leo baada ya mabadiliko makubwa ya pikipiki, WhatsApp, kila kitu vipo karibu karibu sana. Ni bora hizo fedha watupatie tuweke fixed deposit, wataalam watuchoree michoro ya kawaida ya fedha kidogo. Hizi fedha tuziweke fixed deposit, ile interest iwasaidie wagonjwa kwa kuwatibu bure pamoja na chakula. Sasa hivi sisi kule Kanda ya Ziwa tuna-compete na Waganga wa Kienyeji. Haiwezekani wewe una hospitali nzuri haina watu, Mganga wa Kienyeji ana nyumba ya makuti amejaza wagonjwa. Ina maana kuna tatizo pale kwako. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli mimi najua tunachenga chenga, lakini mfungwa ni mali ya Magereza, mhalifu ni mali ya Polisi, huyu mgonjwa ni mali ya nani? Maana yake mgonjwa hana mwenyewe. Katiba yetu inasema, Serikali italinda watu wake na mali zake kwa nguvu zote, kwa hali na mali mpaka na jeshi. Kwa nini hatuna namna yoyote ya kumwokoa mtu anapokuwa anaumwa? Mimi nafikiri nimwulize Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa nini hapo panachengwa? Ila baada ya kifo tunakuwa na misiba, tunakuwa na mambo mengi yanakuja, lakini kwenye dawa hakuna mtu anataka kupagusa wala kwenye matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha alifikirie sana. Nafikiri hili linaweza likawa ndiyo kero kubwa kuliko kero yoyote. Leo hii bei ya dawa/matibabu, wote ni mashahidi humu, sasa hivi umezuka mtindo, unapokuwa na mgonjwa mahututi, wanasitisha matibabu kwa sababu bill imekuwa kubwa. Sasa kama wamesitisha nawe huna fedha, ina maana unatakiwa ukabiliane na kifo. Je, ni sahihi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali haina namna yoyote? Nani tumwombe na nani tumwulize? Hali ya kule vijijini, maisha ni magumu sana, na ugonjwa hauna kusema huyu ni tajiri, huyu ni masikini, huyu ni nani? Mtu yeyote anaweza kuugua wakati wowote. Nafikiri mambo mengine ni kwa ajili ya mabadiliko makubwa ya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, labda Serikali ingefikiria baadhi ya miradi kama mnaweza kuitazama upya, inatakiwa kuendelea sasa hivi au tuishie wapi? Kwa sababu, ninachosema, leo bei ya container kutoka Dubai kuja Dar es Salaam ni dola 15,000, kutoka dola 3,500. Je, hii miradi ikipanda mara nne, tutapata wapi fedha? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami niungane na Wabunge wenzangu kuchangia Wizara hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais, Waziri Mkuu na wewe mwenyewe Mheshimiwa Spika kwa kuchaguliwa kuwa Spika wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kitila Mkumbo na Mheshimiwa Gambo wamejaribu kuliongea vizuri suala hili la kupanda vitu, lakini mimi bado nina wazo. Sisi Waislamu tumeambiwa tukatafute elimu mpaka China ila tusije tukachukua dini ya Wachina. Pia Biblia imesema, “watu wangu wataangamia kwa kukosa maarifa.” Mwenyezi Mungu hakusema wataangamia kwa kutojua kusoma na kuandika, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakisema ukachukue elimu mpaka China, walichomaanisha ni kwamba tukachukue mawazo ya Wachina na siyo maandishi ya Wachina; ila kama una wasiwasi utasahau, unaweza ukajifunza Kichina kidogo ukaandika ili uje ukumbuke huku. Wataalam wetu, wasomi wetu wa Tanzania asilimia 90 wanajua kusoma na kuandika siyo maarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niko kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara. Hapa tunapolia mabati, Serikali inakataa mabati kuanzia gauge 33 mpaka gauge 40, kwa nini? Je, imepiga marufuku nyumba za nyasi? Imepiga marufuku nyumba za tembe? Sasa wewe una shida nyumbani kwako, huna hela ya kuweza kula ugali mweupe, si unasaga dona? Si ndiyo maana yake? Sasa wakati huu wa shida, wewe unakataa watu wasiezekee mabati ya gauge 40 wakati hujatukataza sisi kutumia nyasi. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hii elimu ya kwenu ndiyo iliyotutoa sisi kwenye nyasi ikatupeleka kwenye bati. Ninyi mlikuja mkatuambia kwamba nyumba za nyasi ni mbaya, anzeni kutumia mabati. Leo mabati yamepanda, mnatuwekea sheria tena tusitumie ya gauge 40, kwa sababu gani? Tunamwomba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara atoe hiyo dharura maana bati la gauge 40 ni shilingi 8,000/=, unamkatazaje mwananchi? Leo nyasi hazipo na hawa new generation hawawezi kuezeka nyumba ya nyasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia viwanda vya cement kwenye Kamati vime-confirm vinayo cement ya shingili 5,000. Mheshimiwa Waziri anakataa, anasema wataalam wamemwambia kwamba maghorofa yataanguka. Wananchi wanajenga maghorofa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nimesema kwamba wataalam wetu asilimia 90 wanajua kusoma na kuandika, hawana maarifa. Wananchi kule vijijini wanatulalamikia mno kwamba hivi nyie kweli, ndiyo mmesoma, unanikataza mimi, lakini juu nimeweka turubai navujiwa; umenikatalia bati la gauge 40, inakuja kweli kwenye akili? Haiwezekani! Hata kama mnasema tukaiambie Serikari ipunguze, itapunguzaje sasa? Itafanyaje kupunguza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tulipewa hela hapa za Mheshimiwa Mama Samia shilingi trilioni moja na kitu, zote tumempa Dangote, mmekataa matofali ya kuchoma. Hela si wangebakiza kwa wananchi? Shule za matofali ya kuchoma leo zina miaka 150 na Makanisa yapo. Sasa Dangote kachukua hela, ALAF wamechukua hela ambao ni Wachina, sisi ndiyo tutalipa deni. Kwanini hela nyingine isingeenda kwenye matofali ya kuchoma, wananchi wetu wakapata hela na ndiyo walipaji wa lile deni? kwa hiyo, najaribu kuleta hili wazo ambalo wenzetu wataalam lazima tukubaliane kwamba tuna watu wa hali ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi hapa kama sikosei, ni miezi miwili au mitatu kuna gazeti la Busara lilitoa mwelekeo kwamba taasisi inayoongoza kwa kufanya vizuri sasa hivi, ni Jeshi la Wananchi wa Tanzania ikifuatiwa na wananchi wale wenye mila za kienyeji. Sisi Bunge ni taasisi ya saba kwa kuwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ombi langu, sisi kule Kanda ya Ziwa asilimia 75 ya watu wetu wana dini za mila. Kwa nini Serikali isiruhusu wafundishe na wao dini yao mle kwenye shule? Serikari ipitie vile vitabu vyao, linapokuja somo la dini wanapofundishwa Wakristo na Waislamu, na wao wafundishe. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nasema hivi kwa sababu, hawa watu wako asilimia 75, lakini dini yao ni nzuri mno. Wao wanachofundisha ni kusalimia umepiga magoti kwa mtu mzima, siku ya harusi wanafanyia harusi kwenye mti, wala hamna kadi wala hamna nini; kwenye mazishi mnaleta chakula toka kwa jirani. Je, ni kosa utaratibu huo ukifundishwa; ili siku wakija kufika sasa wenye dini, wakute watu hao ni wastaarabu. Ila sasa hivi, mnachofanya nyie, mnawapelekea kamari na disco. Sasa ipi bora? Wafundishwe utaratibu wao waishi vizuri kwa utaratibu ili siku nyie mkifika na dini zenu, basi wanaweza wakaungana, kuliko sasa hivi tukiwaacha hivyo hivyo na kila mtu anawasakama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Utamaduni alifikirie, maana yake Mheshimiwa Rais sasa hivi mnafahamu ndiyo Kiongozi wa Machifu, sasa Machifu gani kama hawatakuwa na kitabu cha kufundishia wale watu wao?(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia tu, ni suala hili la mtihani. Siku ya mtihani wanakuja polisi, kuna kuwa na vurugu pale shuleni, najaribu kujiuliza hivi kweli mtu toka darasa la kwanza huwa anakuwa wa kwanza mpaka darasa la saba mpaka form one, wewe hofu yako nini mpaka unaleta polisi siku hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini kama matokeo yatakuja tofauti wewe unayemtilia shaka ni yule ambaye huwa wa mwisho, kama wa mwisho amefaulu si uangalie kwenye notice zake tu za kila siku toka darasa la kwanza, kwa nini we leo umefaulu. Kwani akili ya binadamu ni bando kwamba wewe uliweka bando leo siku ya mtihani.(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, sioni sababu maana wale watoto wanakuwa na hofu, wanaona polisi, kunakuwa na hekaheka, ni ya nini, toka darasa la kwanza rekodi zote zipo, kama atafaulu ambaye hafaulu basi, ni kwa nini unafuta mtihani wa shule nzima. Kwa nini usichukue tu wale ambao unaona huwa hawana akili leo wamefaulu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo najaribu tu kuona kwamba wataalam wetu wajaribu kufikiria maisha ya wananchi, wasiwe rigid, kuna mabati ya asbestos, yalipigwa marufuku hapa miaka 40 iliyopita, sababu ilisemwa ni kansa, tunamuuliza Mheshimiwa Waziri miaka 40 iliyopita sababu hizo zipo, wataalam tunao kwa nini wasifanye research tena, maana yake bati la asbestos linatengenezwa kwa mkono, leo nani angelia mabati na unatumia katani na cement linakuwa bati mbona sie tunaezekea matope na nyasi? Ndio tunataka elimu iwe hivyo hatutaki elimu ya kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka elimu ikawasaidie wananchi hasa wakati huu wa matatizo, hata wakisema tumbane Mheshimiwa Rais, wataweza kupunguza bei ya vitu duniani, kwa nini wanakataa tusirudi huko ambako kuna solution ya dakika moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba Waziri atangaze kwamba kuanzia kesho kwa dharura hii tumeruhusu sasa hivi unaweza kutumia mabati ya gauge 40.

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango huo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya wapiga kura wangu wa Jimbo la Kahama Mjini, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kutusaidia sana kwenye ujenzi wa shule na kutupunguzia michango mingi ambayo imekuwa mizigo mikubwa sana kwa wananchi wetu namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili la elimu naona ni vizuri kwa kuwa tunaliongea kwa mapana Mheshimiwa Waziri, ingekuwa dini tungeweza kuhama, lakini kwenye elimu utahamia wapi. Kwa hiyo ingekuwa dini mtu anaweza kuamua hii bwana imenishinda unahamia dini nyingine, lakini kwa mazingira yalivyo kwenye elimu huwezi kuhama. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri wa Elimu ajaribu kutuelewa sisi Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi, hali ya wananchi kwenye suala hili la elimu ilivyo kule vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima Serikali ikubali, ikanunue mawazo na maarifa mepesi ili wanafunzi kuanzia darasa la kwanza, baada ya kuwa wamejua kusoma na kuandika wafundishwe elimu mbadala. Kuwe na elimu hii tuliyoachiwa na mkoloni, lakini tuwe na elimu mbadala. Maana yangu ni kwamba sisi tunaotembea sana nchi mbalimbali, leo hapa mimi nakwenda shuleni nafundishwa panzi ana miguu saba, senene ana miguu minane. Hivi elimu inakataza kweli kuniambia bei ya senene ambayo leo ni Sh.50,000 naishia tu hapo kwa kilo moja, ni kosa?

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunafahamu kabisa kwamba panzi wana protein na wanaliwa na kuku, je ni kosa kufundishwa darasani kwamba kuku anakulaga panzi na kilo moja ya panzi ina panzi 17 na ukimpa utakuwa umesevu kununua chakula cha kuku. Je ni kosa kielimu, kwa nini isiwe kwenye elimu mbadala?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu leo hapa Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi, watu wanaomba kibali zah kuagiza kibali cha kuagiza chakula cha samaki India, lakini wote tunafahamu kwamba samaki anakula minyoo au chambo na kutengeneza minyoo mtu akifundishwa darasa la kwanza inachukuwa masaa 16 kupata minyoo, ni kosa?

Mheshimiwa Naibu Spika, je, unataka mtu mpaka asome, amalize form four, six, akawe fundi seremala atengeneze makochi yasiyonunuliwa, ni kweli tunaenda kuwaambia wananchi wauze ng’ombe, waje wasome waende VETA, waje watengeneze makochi, ni sawa? Wakati elimu yetu inaletwa, dunia haikuwa hii, dunia ilikuwa ni nyingine kabisa, je turudi kwa Waingereza hawa wanaoangalia mpira wa Chelsea na watoto wao, wanaweza wakatukumbuka watubadilishie elimu? Kweli sisi tunashindwa kabisa kufundisha watoto wetu darasa la kwanza wakatengeneza minyoo, wakawapa kuku, samaki badala ya sisi ku-share mahindi na kuku ni kosa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajaribu kuonyesha namna ambayo ni rahisi mtu kuishi. Zamani mtoto wako wa kwanza akimaliza shule, anawachukua wale wadogo zake anakwenda kuwa nao anakuondolea mzigo. Sasa hivi anamaliza degree, anarudi nyumbani, je, wewe utakuwa na moyo wa kuwasomesha hao wengine una moyo gani huo?

Mheshimiwa Naibu Spika na Mheshimiwa Waziri utakuwa na moyo huo wakati huyu kwanza hajapata ajira, ng’ombe wamebaki nusu, utakubali uuze ng’ombe waliobaki umsomeshe na huyu abaki nyumbani? Haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima viongozi wakati huu wa shida ya mabadiliko duniani ndipo ambapo viongozi strong huonesha mabadiliko makubwa sana ya kwenda mbele, kuliko tukisema na sisi tuwa-damp wananchi na sisi wote tunao watoto kwenye masofa, wamejaa wameweka masikioni wanasikiliza na wanacheza na WhatsApp. Je, tuendelee kuwa- damp hivyo? Je, wale panya road au panyabuku tutawaweza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani! Wenzetu Wizara ya Elimu wanayo maabara mle ndani. Kweli maabara inashindwa? Leo Mheshimiwa Bashe analia mbolea, kweli shule ishindwe kufundisha mtoto kutengeneza mbolea ya kienyeji ambapo ni kuchukua nyasi na udongo na kumwangia maji na kuuza barabarani, hata kama kilo moja shilingi 300, mtoto huku anasoma, lakini Serikali na sisi tunapata mbolea. Hili pia linahitaji kweli mpaka tujue tu Kiingereza, TEHAMA; je, ng’ombe pia tutachunga kwa TEHAMA kweli? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, je, kama tunavyotaka ni hivi, ni kweli wote tutasoma tumalize wote tuwe na degree, tutoke na ng’ombe kule Kijiji tuzilete mjini tena, tuje nazo huku tumesoma, tunaongea Kiingereza. Itawezekana kweli! Kwa hiyo, tunamwomba Waziri wa Elimu ajaribu na Kamati yake kuona kwamba hawa tunaowaongoza ni raia wa kawaida kabisa wenye maisha ya chini, wanahitaji elimu ndogo ya kujishikiza huku wanaishi ili Serikali inunue mawazo mepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli suala hili linatupa wakati mgumu sana kiasi ambacho unapokwenda kule vijijini, wazee wanatuuliza: “Hivi kweli hakuna njia yoyote ya nyie kufikiri?” Nasi tukirudi kwa wenzetu huku wanapiga tu stop kwamba haiwezekani. Kama leo inapatikana teknolojia duniani, Waziri wa Elimu si aingize tu kule kwenye simu awaeleze kule walimu kwamba jamani, sasa hivi ukichukua lita moja ya maziwa ukatikisa saa moja, kinachopatikana ni mafuta ya kula. Hata hiyo nayo ni kosa kufundisha shuleni? Sasa nani tumwite aje atukomboe? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunalia mafuta, watoto wetu hawajui kama kwenye maziwa kuna mafuta, itawezekana kweli tusomeshe watu; ukimwona mtoto aliye na degree, ukimweka mahala, ni kama umemweka kuku wa kizungu. Unamwona kweli huyu mwanangu sijui nitamkuta, sijui atagongwa, sijui atanyang’anywa hili begi alilonalo! Ni kazi ngumu kweli! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, kweli teknolojia inakataza kitu chenye faida? Inakataza kabisa, haiwezekani! Yaani teknolojia ni lazima iwe kutengeneza magari na ndege tu; na TEHAMA? itawezekana kweli! Yaani Tanzania nzima, watu milioni 60 wataenda kwenye TEHAMA? Wataziunga wapi hizo computer? (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata shule ya msingi, mmesema hapo wenyewe, kuna wanafunzi 400 mle ndani: Je, wangekuta asubuhi wanafundishwa kutengeneza minyoo, si wangekuwa wanauza pale nje wakati wanamsubiri mwalimu? Wafugaji wa kuku wangenunua. Si ndiyo sawa tu, tutafanyaje? Dunia imebadilika, population imeongezeka, watu wanahitaji vyakula: Je, tuendelee na procedure ya mbao? Mheshimiwa wa Maliasili naye anataka miti yake, watu wasome wawe mafundi seremala na mafundi rangi. Tanzania nzima tutakuwa mafundi rangi! Haitawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunamwomba sana mwenzetu Mheshimiwa Waziri wa Elimu ya Juu, ajaribu hata yale mawazo ya local. Mpaka wafugaji wanatuuliza kwamba ah, usiniletee maneno ya shule hapa, ng’ombe zangu zilizobaki hizi, mpaka nife mwenyewe, siwezi. Sasa tukatae ukweli, kwani nani hajui?

Mheshimiwa Naibu Spika, wote si tunafahamu kabisa kwamba sasa hivi mtu aliyesomesha kule kijijini ndio anayechekwa. Kwa sababu watoto hawawezi kulima, hawezi kufanya kazi yoyote na ng’ombe zimeisha, naye amezeeka, anaandikisha TASAF, itawezekana kweli? Sasa mbona kuna elimu ndogo na nyepesi ambayo inaweza kutusaidia kwenye huu muda ambao tunao kuliko kung’ang’ana tu kama Waingereza. Maana yake tukiongea wote kama Waingereza, kweli wale Waingereza wa Liverpool watakuja kutusaidia kweli! Itawezekana kweli watuletee mawazo mengine ya kutukomboa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo, namwomba tu Mheshimiwa Waziri asipuuzie, maana yake mtoto kwenda shule ni kwenda kuanza mawazo na maisha mapya. Akitusaidia kutufundishia watoto wetu hizi kazi ndogo ndogo za kawaida, atakuwa ametusaidia sana wakati wanajiandaa kwenda kule mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nami nampongeza Mheshimiwa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri na watumishi wote wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaliongea kidogo suala la CAG, lakini siyo kwa tarakimu. Suala hili la CAG linatupa wakati mgumu sana na sioni kama kuna uwezekano tutakwenda labda miaka 10 wizi hautaisha. Labda tutafute namna ambayo ni nyepesi kidogo. Kwa nini CAG anakagua baada ya tukio? Kwa nini CAG asianze kabla ya mradi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yangu ni kawaida mbwa huwa anabweka wakati kuna mwizi ili mwenye mali atoke, lakini mbwa akibweka baada ya kuibiwa, kuna uwezekano kwamba mbwa hakuwepo kwenye eneo lile. Kwa hiyo, tumwombe Mheshimiwa Waziri Mkuu, kama itakupendeza, tuwe na Wizara ya Matumizi na Wizara ya Kero. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, anayetayarisha mradi ni Katibu Mkuu na watumishi wake kwenye Wizara au sisi Halmashauri. Tunashauriana kwa sababu ya pesa zilizopo, tunaamua tufanye mradi. Hapa kwenye mradi, anachoangalia CAG ni kile kilichotoka nje ya ule mradi, lakini asilimia 80 ya miradi ile haina mahitaji yoyote kwenye jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano wa masoko yetu. Ni kweli, soko la ghorofa unatarajia kweli ujenge soko la ghorofa uweke nyanya watu wakanunue na umetumia shilingi bilioni 30; haiwezekani! Yaani tubishe, yaani tuone kabisa, tunaona soko la kawaida liko mahali pale, unaweka soko la shilingi bilioni 40 kwenda kuweka nyanya na samaki, watu watafuata kweli kwenda kununua? Kama kungekuwa na Wizara ya matumizi, huu mradi ungepelekwa kwao, wakauangalia kwamba huu mradi; je, unafaa? Kama wanaona unafaa, wampelekee na CAG na TAKUKURU wauangalie ndiyo uje Bungeni. Ingekuwa muda huu tunazozana fedha hazijaenda, lakini sasa hivi tunazozana pesa zimekwenda, tena tunaidhinisha bajeti nyingine. Tutafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunaiona miradi yetu asilimia kubwa haina faida kwa wananchi, badala yake tena inakuwa kero. Leo unabebwa kutoka hapa unaambiwa huwezi kuteremka na basi hapa na mvua inanyesha, lazima uende mwisho kwenye stendi ya Nane Nane. Umetoka Bahi, ni shilingi 5,000 kuja hapa. Ukiteremshiwa Nane Nane kurudi tena huku, ni shilingi 10,000. Huyu mwananchi tunamwadhibu kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo utatengeneza mradi; huo mradi wako ulichukua hela zetu, ukatengeneza mradi mbaya, halafu leo unatuadhibu sisi tena wenye hela. Tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu alifikirie kwa mapana sana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nimemuunganisha Waziri wa Matumizi na Waziri wa Kero? Nafikiri mmeona hoja hapo ya Mheshimiwa Kunti ilivyokuwa. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri Mkuu, inatupa wakati mgumu sana sisi kukabiliana na Mawaziri kwenye matatizo ya hoja, lakini kama kuna Waziri wa Kero, sisi tutapeleka kero zetu kwake yeye, yeye ndio atazipeleka kwa Waziri Mkuu. Maana yeye hahusiani na kitu chochote, ni kama Waziri asiye na Wizara Maalum. Itatusaidia sana. Kuna kero nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunalia ajira. Leo daktari anamaliza University Muhimbili, anakuja hana kazi, lakini haruhusiwi hata kufungua kiosk kuchoma watu sindano, lakini Mmasai anatembeza dawa na ana kibali cha Wizara ya Afya. Sasa tunafanyaje? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu umechukua milioni yake 40, baadae ukamfunga pingu, haruhusiwi tena kuuza dawa, lakini mtu ambaye hakusoma, anatembeza dawa. Samahani ndugu zangu Wamasai kama mpo. Anatembeza dawa, tena anakwambia inatibu magonjwa 40, unakuja saa ngapi? Sasa unafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima twende upya. Mabadiliko ni makubwa sana duniani. Lazima tufungue vitu vingi sana, kero ni nyingi mno. Leo wote humu ni mashahidi. Tunapanda ndege kutoka hapa Dodoma kwenda Dar es Salaam, hapa unasachiwa, unafika Dar es Salaam unasachiwa tena. Je, ulipakia abiria huko angani? Nani alipanda angani? Sasa tutamwambia nani? Hakuna wa kumwambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaenda barabara yetu ya mwendokasi. Mwendokasi unaona ziko nne, upande huu kuna daladala zaidi ya 100, lakini haziruhusiwi kuhamia huku, lakini huku hakuna watu, lakini nao si wanalipa deni hilo hilo! Mvua inanyesha, wamo mle kwenye daladala wameshika mkono, kwa nini wasiruhusiwe watu wa daladala wakatumia hii kwa muda mpaka tutakapopata mabasi? Maana hawa na wenyewe si wanalipa deni. Je, ikitokea mwenye funguo za ofisi yuko kwenye daladala, wewe wa mwendokasi ukawahi, faida ya mwendokasi itakuwepo? Si utakuwa mlangoni! Haitawezekana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, najaribu sana kufafanua kwamba, akiwepo Waziri wa Kero na Waziri wa Matumizi, sasa hivi ndiyo ungekuwa muda wetu kubanana kwamba, mradi huu tumeukubali uende, mradi huu bwana kama unataka kuuza nyanya kwa shilingi bilioni 20 hatutaki. Katengeneze banda la shilingi bilioni tatu, wanunuzi wa nyanya watanunua. Kwa hiyo, tunge-save sana. Huu mvutano wote usingekuwepo. Nafikiri mnafahamu kesi ya CAG ilivyowahi kuleta matatizo mengi mno kwenye Serikali. Mengi mno!

Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa hiyo, tukuombe ulifikirie kwa makini sana. Pia bado najiuliza, Serikali imeamua kurudi kwenye biashara. Kilichoifanya ikatoka miaka ya 1980 na miaka ya 1990 kimebadilika? Watu wa miaka ya 1990 na 1980, na hawa wala blue band wa leo, kama wale walishindwa waliokuwa wanakula mihogo, hawa wala blue band wataweza biashara? Kweli tumeamua kurudi kwenye biashara? Kweli tutaweza? Kwa haya matatizo tu yaliyotokea haya ya wizi, tunarudi kwenye biashara tena za gharama kweli, tutaweza kuziendesha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiwaona matajiri, asilimia 80 hakuna mzima. Mwingine ana gout, mwingine ana pressure, yaani kutwa nzima makoti yamejaa vidonge: Je, itawezekana kweli! Au kwa kuwa, Serikalini ninyi mnastaafu miaka 60, mnataka kumtelekezea nani huo mzigo? Maana mzigo huo ulishatelekezwa miaka ya 1990, tukauza na viwanda, tukasema jamani tunatoka, sisi tunarudi kwenye kodi, lakini immediate tunaenda moja kwa moja tena kwenye biashara. Kabla hatujaanza biashara, nusu ya hela imeibiwa. Sasa hiyo biashara tutaianzaje? Nani atatuletea hela? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa hiyo, tunaomba sana hili suala la CAG tubadilishe huu utaratibu ili tujadili hela kabla ya wizi wenyewe. Baada ya hapo, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniaptia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Kilimo. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuongeza bajeti kwa 29 percent kwenye bajeti yetu ya kilimo, ambayo itatusaidia sana hasa sisi ambao tunatoka katika maeneo ya kilimo. Mwaka huu tunakabiriwa na ukame mbaya sana ukilinganisha labda wa mwaka 1974, kwa hiyo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tunahitimisha Wizara ikiwemo na kamati moja, mimi leo nitaanzia Wizara ya Mifugo na uvuvi ambayo ilianza mwanzo.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri Mwanasheria Mkuu wa Serikali yupo hapa; tunaomba, kwa wafugaji wetu ambao ng’ombe wao wamekamatwa kwenye hifadh,i wanapokuwa wametolewa hukumu wapelekwe kwenye mnada kwenda kuuzwa kihalali badala ya mtindo wa sasa hivi ambapo watu wa kule hifadhi wanapiga mnada wao. Wapelekwe mnadani kama sheria ya Serikali ilivyo na mnada wa Serikali ndio unaotambulika, itawasaidia sana. Wafugaji wetu watapata kinachobaki na wao Serikali watapata kinachobaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la kufunga Ziwa Tanganyika na Ziwa Victoria. Sisi maeneo yetu uchumi wetu pia unategemea maziwa haya. Maziwa haya yakifungwa tutakuwa tumeingia kwenye mgogoro mkubwa sana hata sisi watu wa Kahama na Shinyanga, hasa wakati huu ambao ni mgumu sana kwetu.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze Wabunge wa Kigoma kwa mchango mzuri sana ambao walionesha wakati wa kutetea. Lakini kikubwa, na hoja yangu ya msingi hapa ni kwamba lazima wataalamu wetu watumie muda mrefu sana wa kufikiri. Ng’ombe anazaa mtoto mmoja kwa mwaka, mbuzi anazaa mtoto mmoja kwa mwaka, na kondoo pia, lakini hatujawahi kuona shortage inatokea. Ni lini tumepata shida kwamba nyama ya ng’ombe hakuna au ng’ombe hakuna; na hata sasa hivi tunazozana kupunguza ng’ombe?

Mheshimiwa Spika, samaki anazaa watoto laki mbili mpaka milioni moja; tunahakika wamekwisha? Ni uongo wa mchana. Kinachoendelea hapo ni kwamba gharama ya uvuvi imepanda. Leo drum moja la petrol ambalo ni lita 200 unahitaji zaidi ya shilingi 800,000 mpaka 1,000,000. Sasa kama una ma-drum matano unaondoka kwenda kuvua huna darubini, hujui samaki walipo, umeondoka na gharama ya shilingi milioni tano, unategemea utapata samaki wa milioni nane? Haiwezekani, ni report za uongo.

Mheshimiwa Spika, je, hawa wangekuwepo siku Yesu alipowakuta akina Simon na Petro wamekosa samaki wangelifunga Ziwa la Galilaya? Uvuvi ni kubahatisha; haiwezekani kazi ya kubahatisha, hakuna uvuvi duniani asili yake ni kubahatisha. Hata siku ya Bwana Yesu alikuta akina Simon na Petro wamekosa Samaki ndipo akawaombea wakapata. Sasa angekuwepo mtaalamu wetu angelifunga Ziwa la Galialaya? Haiwezekani, hatuwezi kuwa na wataalamu ambao ni wavivu wa kufikiri, watatuingiza kwenye migogoro mikubwa mno. Mnaona tunazozana hapa suala la herein, tunazozana kweli wananchi mpaka wanauliza, kwa nini ninyi huwa hamleti mijadala ya kutupa nyasi za kulisha ng’ombe? Ninyi mijadala yenu yote ni kuja kwetu kuja kutukamata. Hakuna mawazo mapya yanayotoka kwenu? Wananchi wanahitaji mawazo mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakwenda kwenye suala la kilimo. Ni kweli kwenye jimbo langu nina viwanda zaidi ya sita vya pamba na vinategemea pamba, lakini kwa bei inayoonesha, ya mwaka huu, labda tu tumuombe ndugu yangu Mheshimiwa Bashe mbegu za pamba na viuatilifu vya pamba viuzwe madukani kama zilivyo mbegu za mahindi na mazao mengine, itatusaidia. Kwa sababu sasa hivi mwananchi atakatwa shilingi 490 mpaka 500 kwa kilo moja, Mheshimiwa Bashe ni huruma na huruma, lazima ufanye huruma ngumu sana. Mwananchi anapata kilo 200 kwenye ekari moja shilingi laki mbili; akikatwa huyu mtu, na hali ya chakula ilivyo, ni lazima kufikiria sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, ruhusu watu wanaoweza kununua mbegu zao wanunue ili wao wakati wanauza pamba yao wawe huru kama mazao mengine. Kwa nini mimi mnanilazimisha nikaungane kwenye group lingine? na kwa nini mimi nimlipie mtu ambaye mimi sihusiani naye? Mimi nimelima pamba kidogo, sikutumia dawa, sikutumia mbolea, nimelima na wanangu, naendaje kumlipia mtu mwingine aliyetumia mbolea na dawa? Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, trend hii ikienda zao la pamba tunakwenda kulinawa, a hundred percent tunakwenda kulinawa; kwa sababu mazao ni mengi mno Kanda ya Ziwa. Alizeti leo heka moja mtu atapata shilingi laki saba au nane kwa nini akalime pamba yenye matatizo mengi na migogoro mingi? Halafu ndiyo iwe na sheria kali. Kwa hiyo namuomba sana Mheshimiwa bashe aliangalie kwa mapana sana suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni suala la mbolea hii ya kupima. Mheshimiwa Waziri yeye ana bucha; sasa nashangaa; wewe Mheshimiwa Bashe kwenye bucha lako unapima nyama watu wanaenda kula; sasa unamkataza mtu kupima mbolea ikaende ardhini, inawezekana kweli? Yaani haieleweki ni kwa nini. Na ukiisoma hiyo sheria ya kupima mbolea ni miaka miwili jela? Sasa, mwananchi hana hela laki moja na nusu, anataka kulima mchicha, sasa anafanyaje? Au unataka kuweka kwenye garden? Kwa nini mbolea iwe na thamani kuliko chakula? Wote tunaona, sukari tunapima.

Mheshimiwa Spika, karibu na kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu pale kuna nyama za kuku ziko nje, tena zimechomwa na Waheshimiwa Wabunge wote mko pale. Sasa iruhusiwe kula nyama iliyochomwa iko nje lakini mtu anayechukua mbolea kusaidia mwenzie anakamatwa matokeo yake wananchi wanauziana kwa magendo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri aruhusu, hizi sheria mengine za kikoloni kwa sasa hivi hatuzihitaji tena. Kama mama ametoa fedha zote hizi tunaendeleaje na sheria mbaya za kikoloni?

Mheshimiwa Spika, Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Viwanda na Biashara anafahamu vizuri. Kuna sukari ambayo inatengenezwa kutoka kwenye viazi vya kienyeji; na hoja hiyo imeletwa mara nyingi sana kwenye Kamati wakati mimi bado niko kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara; na sukari hiyo ni sukari ambayo inatumika kwenye soda na vitu vingine, hata kwa chakula, na ni nzuri mno, lakini inapigwa vita na watu wa viwanda vya sukari. Kwa sababu wananchi wakianza kulima viazi hivi vya kawaida wakatengeneza sukari teknolojia hii itawaondoa wao kwenye miwa.

Mheshimiwa Spika, leo mmesikia mabadiliko makubwa yaliyotokea China, China nusu wanatengeneza gari za umeme. Si na sisi tutatupa gari zetu huku? Kwa nini wao wazuie wananchi wasilime viazi ambavyo vinaiva miezi miwili, havihitaji dawa na havihitaji kitu chochote ili wakatengeneza sukari, lakini baada ya makapi yale yakawa ni chakula? Sasa kwa nini watu wakatae kibabe, kwamba wamekataa?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Khenzile ni shahidi, anafahamu, wafanyabiashara wamekuja mle wanalia, kwamba jamani ruhusuni viazi hivi vya kawaida.

Mheshimiwa Spika, maana sisi hata kwa kienyeji viazi ukivikausha ukaja ukavichemsha inayotoka ni sukari, wala haina hata ubishi. Kwa hiyo ni kiasi cha Wizara ku-promote ili kuondokana na hili la kulalamikia mazao ya kila aina.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia nimshukuru sana Mheshimiwa Bashe, umetusaidia sana hasa wakati wa njaa. Ametusaidia mahindi ya kutosha na kila wakati tulikuwa tukihitaji msaada wowote amekuwa akitusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango huo nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Bajeti ya Wizara ya Fedha. Nami namshukuru Mheshimiwa Rais, Waziri wa Fedha na timu yake nzima kwa kuleta bajeti kwa ajili ya Wizara yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikiliza Mheshimiwa Kilumbe hapa akiongea suala la dola na pia kulikuwa na swali asubuhi. Sisi kwetu kwenye majimbo yetu ndipo yalipo masoko ya dhahabu. Soko langu la dhahabu kwenye Mji wa Kahama, kutoka benki zilipo ni mita 50. Sasa najaribu kujiuliza, hivi kweli unaweza kuwa una soko la dhahabu inayochimbwa na wenyeji na ukasema tena hauna dola kwenye mita hizo hizo? Inatupa wakati mgumu sana wa kufikiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata Mtemi Mirambo wakati Waarabu wanakwenda kuchukua pembe, wakija na pembe kumi, alikuwa anachukua mbili. Wakitoka huko na bunduki, anachukua bunduki mbili na yeye, badaye wanabadilishana. Sasa wewe unachukua dhahabu, unai-charge shilingi. Milambo alikuwa anachukua pembe kumi. Kwa nini usikate hata kipande cha dhahabu ukapata dola? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tulie kabisa kwamba hatuna dola? Soko la Geita linaongoza leo kwa dhahabu, lakini dhahabu ni dola. Kuna tofauti gani wewe unanunua ndege, inafuata watalii China, inawaleta mpaka Ngorongoro, wanakuja unawatengenezea na chakula, ndiyo wanakupa dola, lakini unakataa dola inayochimbwa kama mihogo kuja nyumbani kwako, unakataa! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani Mheshimiwa Waziri alifikirie kwa mapana sana. Maana yake kwa muda tunao-delay inaweza ikatuweka kwenye matatizo makubwa, maana watu wanapata riba wakati wanasubiri dola. Pale kwangu Kahama mimi mwenyewe nimetafuta Dola 1,000 nimeshindwa kupata, lakini opposite yake kuna tani za dhahabu. Tuombe tu wenzetu wa Wizara ya Fedha waondoe huo uoga. Wanaogopa nini? Huwezi kuwa na dhahabu ukasema huna dola, haiwezekani. Kwa kweli ni kitu ambacho kinatuhuzunisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala hili la share. Share, ni Wazungu walikaa miaka 100 iliyopita kule Ulaya wakatengeneza huo utaratibu. Utaratibu huo ulivyo sasa hivi, kuna migogoro mingi sana. Nitatoa mfano. Shirika la Ndege la Precision watu wamenunua share, watu wamenunua share hata za Voda, za Tanzania Oxygen, lakini mpaka leo hakuna pa kuuza hata kama unaumwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndege ya Precision inakwenda Mwanza, ina nafasi kumi ambazo hazina watu. Kwa nini mimi mwenye share siruhusiwi kukata against share kwenye ile tiketi ili wakakata kwenye ile share? Kama wewe unasema kwamba mali hii ni ya kwangu, unakataaje? Mimi nina share kwako, kwani mimi nikinunua ng’ombe kwako, si zinagongwa tu mhuri kwamba hizi ni za fulani, akija saa yoyote mpatie. Haiwezekani! Maana yake mtu amenunua share. Leo Voda anachenga hapa wakati alichukua hela za watu, sasa kama hawezi kuuza share, si tukate kwenye vocha? Awe anatukata kwenye vocha, yeye anachukua zile share? Ni kama vile tulimkopesha. Hilo nafikiri, pamoja na kwamba inaonekana utaratibu ni mgumu, lakini wenzetu lazima walifikirie.

Mheshimiwa Naibu Spika, pana suala gumu sana hapa, Mheshimiwa Dkt. Kimei anafahamu. Sisi na Mheshimiwa Dkt. Kimei tumeteuliwa kwenye Kamati ya kuanzisha Benki ya Wachimbaji, lakini kuna mgogoro ndani ya hili suala. Kule Mwanza tulianzisha Mwanza Community Bank, ikatayarishwa vizuri na tukachanga zaidi ya Shilingi bilioni mbili na kitu, lakini ilivyokuja Sheria ya Benki Kuu, inasema wewe kama huna elimu au hukusoma elimu hii ya fedha huruhusiwi kuwa Body of Directors kwenye ile benki.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi nimekusanya Shilingi milioni 500, halafu nimetoa kwenye benki kama nanunua share, naambiwa siruhusiwi kuwa kwenye Body of Directors. Sasa kwani kupata Shilingi milioni 500, kwa nini usiandike hizo CV zangu kwamba aliuza miwa, mihogo akauza hiki, akapata Shilingi milioni 500! Kwa nini usii-convert hiyo ikawa ni degree au elimu, ukaniruhusu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikupe Shilingi milioni 500, wewe uje na tai na cheti cha degree, nikukabidhi fedha zangu, itawezekana kweli! Tukajitoa na Simiyu Community Bank na yenyewe hivyo hivyo wote tukajitoa, tukasema haiwezekani, lazima mbadilishe, mturuhusu tusimamie fedha zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo najaribu kumwuliza Mheshimiwa Waziri, tutafanya nini kwenye hii benki ya wachimbaji? Mtawapata wachimbaji wenye degree! Mmeshawaambia au mtazua mgogoro tena! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi wameshachanga zaidi ya bilioni mbili juzi Arusha lakini mmeshawaambia kwamba sheria ya kuwemo kuja kuchunga hela zako lazima uwe na cheti cha degree ni sahihi kuchunga hela zako. Haiwezekani lazima wenzetu wa Benki Kuu waangalie kabisa, mbona nyie benki zenu ambazo zinaangaliwa na wasomi si nazo zinaongoza kwa ku-collapse, hazi collapse za wasomi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimeweza ku-raise hela sasa hawa wachimbaji wame-raise hela za Mheshimiwa Doto, wame-raise hela zao, halafu wewe hela ziko tayari unaniambia hauruhusiwi kukanyaga humu, sisi tutakuwa tunakula nyie mnatitizama kule, itawezekana kweli? Haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamuomba Mheshimiwa Waziri na Gavana walifikirie kwa mapana sana ili waruhusu watu waingie wenye hela zao, kwenye board of directors kwenda kuchunga pesa zao. Kwa hiyo, nitakuwa na hela kweli Mheshimiwa Lusinde nishindwe kusaini kujua kwamba huyu ni mwizi na huyu ni mtapeli hatarudisha hela, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, narudia tu kumpongeza Mheshimiwa Waziri nashukuru sana naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi kuchangia kwenye Wizara hii ambayo ni mpya kwetu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri hasa kwa dawati la jinsia ambalo linasaidia sana hasa majimbo yetu ambayo yana watu wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala sasa hivi linatutatiza sana hasa vijijini na sielewi kama suala hili ni sheria au ni utaratibu na uzuri Mheshimiwa Waziri alikuwa Waziri wa Afya kwa muda mrefu kidogo. Suala hili linaleta mgongano sana hasa kwenye jamii zetu za kienyeji, suala la kwenda na kinamama wajawazito na wanaume zao kliniki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unaposema mtu wa kijijini aende na mke wake kliniki unaleta taharuki kubwa sana kwa sababu kwa mila zetu na kwa dini zingine unaruhusiwa kuoa wanawake mpaka wanne na huwezi kuwaoa kwa wakati mmoja. Sasa kama mtoto wako wa kwanza wa mke wa kwanza ana mimba na huyu wa kiume naye mke wake ana mimba na mke wako mdogo ana mimba; je, mtakwenda wote kliniki na siku ya kliniki ni siku moja tu kwa wiki itawezekana? Lakini kwa mila zetu mimba kwetu siyo ugonjwa, ila inapokuwa limetokea tatizo ambalo ni mara chache sana na hata mimba ukiwa unamsalimia mtu mjamzito kawaida huwa tunamuuliza tu vipi mwenye mzigo ameutua au bado? Anasema bado hajatua mzigo, siyo ugonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa pole pole inaanza kuwa kero, kule kwangu Kahama yamewekwa mabango ya watu kukodisha wanaume wa kwenda nao kliniki kwa sababu wanaume wanakataa na je, sheria hiyo ni sheria model gani? Wewe ni mwanasheria, anayeenda kuadhibiwa pale hospitali ni yule mwanamke, lakini atatakiwa aje na mume sasa mwenye kosa ni mwanaume aliyekataa na kwa mila za kwetu mtu anakataa anasema mbona hii kitu sisi hatutaki anayeteseka ni mwanamke, matokeo yake inasababisha mpaka vifo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu huyu mama hana uwezo wowote wa kujieleza, tuelewe watu wetu tunaowaongoza ni watu wa hali ya chini sana, tunapopewa utaratibu na wazungu lazima tuwe tunauliza wazungu jamani hiki kitu unakipeleka kule Afrika na hasa kwetu Tanzania wataweza watu wetu wa kule kijijini kufanya hiki kitu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, humu ndani kuna Wabunge akinamama na wengine ni wajawazito, ukimuuliza tu humu ndani kwamba hii mimba shemeji ni nani hamsalimiani mwezi. (Makofi/Kicheko)

Sasa watunga sheria hawataki kuitekeleza, tena unamuuliza tu na ninajua kama ingekuwa wanafanya hivyo Wabunge tungeona wamejirusha kwenye WhatsApp sijaona hata siku moja Mbunge mjamzito amejirusha kwenye WhatsApp akiwa kwenye bench la kliniki na mumewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri inawezekana ni sababu kubwa pia inayosababisha kuwepo kwa mlundikano wa kesi kwenye dawati la jamii, maana yake unapokodishiwa mke na jina anaenda kuandika yule mume, je, ikitokea yule mtoto akazaliwa yule mume aliyekuwa anampeleka mke akamkatalia mtoto, utafanyaje? Haitawezekana, tumuombe Mheshimiwa Waziri alitizame kwa makini sana hili suala linasumbua mno.

Mheshimiwa Spika, suala lingine tumesema kujifungua akinamama ni bure, lakini ukweli siyo bure, sasa hivi imezuka kama iliyokuwa kwenye shule imehamia hospitali, anaambiwa aje na vitenge pair saba, aje na beseni, aje na gloves, anaambiwa vitu vingi sana. Kwa hali ya sasa ya maisha ya kijijini na hali ya watu wetu ni sahihi kweli na je, watoto wa sasa hivi ndiyo wamebadilika? Ni kitu gani kimetokea hapa katikati ambacho mtoto wa sasa hivi anahitaji vitu vingi namna hiyo na uzuri Mheshimiwa Waziri yeye ni daktari, ajaribu kutueleza kimetokea kitu gani hapa katikati maana yake akifika pale hospitali kama hana vile vitenge, aidha, atoe rushwa au aambiwe kanunue vitenge kwenye eneo lile, lakini kitenge kipya kinaweza kubeba mtoto mchanga kweli? Haiwezekani, ni lazima iwe nguo iliyotumika.

Kwa hiyo, tumuombe Mheshimiwa Waziri aliangalie sana hilo suala kwa sababu linatupa wakati mgumu sana na hasa sisi kwenye majimbo ambayo yana watu wengi sana kwa ajili ya shughuli za migodi na ukulima na ufugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka miaka ya 1985 wagonjwa walikuwa wananywea dawa hospitali, ilikuwa mtu hawezi kupewa vidogo ili aende akanywe nyumbani na wakati ule hospitali zilikuwa mbali mbali na barabara hazikuwepo, pikipiki hazikuwepo, teknolojia haikuwa hiyo, lakini kwa utafiti hata ukiangalia leo asilimia 70 au 60 ya dawa watu hawamalizi dozi wanakunywa, wakipona wanaziacha mle ndani, kwa nini Serikali isirudishe utaratibu wa zamani ili wagonjwa wa vijijini wakanywee dawa hospitali ili kusudi inawezekana dawa nyingi tunapoteza bure na tunakataa kuwatibu watu bure. Kwa sababu mimi ninafahamu mtu mpaka leo anaweka alarm kwenye simu ya kujikumbusha kunywa dawa hasa wagonjwa wale ambao ni wa kisukari au pressure, lakini wagonjwa wengine baada ya kuwa wamepona hasa kijijini mgonjwa anapimwa kwa kuweza kunywa uji, ukinywa uji tu ukamaliza au ukala wanakwambia twende shambani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa hiyo, madawa mengi yanashinda tu kule ndani, kwanini sasa Serikali isiruhusu watu wakanywee dawa hospitali ili mimi kama nimeandikiwa sindano tano, mimi ni mtu wa kijijini nikichomwa mbili nikaona nimepona, mimi siendi, maana yake hata ukinipa dozi nyumbani kwani wewe unakuja kunithibitishia mimi kama nazimaliza, hakuna mtu anayenifuata kama nimemaliza dawa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tungemuomba kwa kuwa sasa zahanati ni ni nyingi na barabara ni nzuri na ni kila kijiji turudishe huo utaratibu kwa sababu pia utatuondolea mgogoro wa dawa fake na kama dawa zitanywewa pale hospitali sidhani tena kama kutakuwa na kesi ya dawa fake na itakuwa vizuri zaidi kwa sababu ukweli kabisa wote tunafahamu kwamba dawa nyingi sana zinabaki majumbani hasa huu tumepita muda wa corona mtu ananunua dawa hii akinywa vitatu, amepona typhoid mpaka inadawa 50 lakini mtu anakunywa nusu siku ya tatu anaachana nazo, kwa hiyo, zipo tu ndani. Kwa hiyo, inaweza ikaisaidia hata Serikali pia kupunguza baadhi ya gharama bila sababu yoyote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kumalizia tu nimuombe Mheshimiwa Waziri aliangalie hili suala kama labda tulijaribie kwenye maeneo ya ndugu zetu labda Tanga na Pwani ili wao waruhusiwe kwenda na wake zao, lakini sisi kule ni ngumu, huwezi kuwa unatoka kulima, utoke kulima na siku ya kliniki ni moja, je, nani atalinda mpunga shambani haitawezekana, maana hamuwezi kwenda wote kliniki mkapangane kweli kwenye fomu wewe na watoto wako na mkwe wako, mpangane hapo kweli na nguo zenyewe za shida aangalie tu kama mimba ina tatizo aniite mimi mwanaume ili mimi niende siku hiyo kwa special maana yake haiwezekani mimba zote zina matatizo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JUMANNE K. KISHIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)