Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Juma Hamad Omar (2 total)

MHE. ABDALLAH A. MTOLEA (K.n.y MHE. JUMA HAMAD OMAR) aliuliza:-
Kumekuwa na utaratibu wa muda wa kulipa malipo ya pensheni kwa wastaafu kama vile kila mwezi, kila baada ya miezi sita na kila baada ya miezi mitatu.
(a) Je, ni utaratibu gani kati ya hizo zilizotajwa hauwasumbui wastaafu?
(b) Je, ni formula gani inayotumika katika kuwaongezea wastaafu pesheni zao ili angalau kwa kiasi fulani ziweze kusaidia kukidhi maisha yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Hamad Omar, Mbunge wa Ole, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu mzuri wa kulipa mafao ya pensheni ni malipo ya kila mwezi. Aidha, malipo ya pensheni yanaweza kutafsiriwa kama malipo mbadala ya mshahara wa kila mwezi kwa mfanyakazi aliyestaafu. Ni wazi kwamba malipo haya yanakuwa na mahusiano makubwa na maisha ya kila siku ya mstaafu kama ilivyo kwa mshahara ama kipatao kingine kinachotokana na maisha ya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kutokana na hali halisi ya mazingira ya nchi yetu kijiografia na gharama za kufuatilia pensheni husika, baadhi ya mifuko ya pensheni iliweka utaratibu wa kulipa kwa mafungu ya miezi mitatu au sita ili kupunguza gharama kwa wastaafu. Aidha, kutokana na maendeleo ya teknolojia natoa rai kwa mifuko yote kuendelea kuboresha mifumo yao ili kuendelea kutoa mafao kwa wakati kadri inavyowezekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, utataratibu wa kuhuisha pensheni, indexation umebainishwa katika kifungu cha 32 cha Sheria ya Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii, Sura ya 135, kikisomwa pamoja na kifungu cha 25 cha sheria hiyo ambacho kinaitaka mamlaka kufanya tathmini ya mifuko husika kabla ya kutoa viwango vya mafao, kwa mfano, kufuatia tathmini ya mifuko yote iliyofanywa katika kipindi cha mwaka 2015/2016 mamlaka ilikwishatoa maelekezo ya viwango vipya vya malipo ya kima cha chini cha pensheni ya kila mwezi kwa mifuko yote.
MHE. JUMA HAMAD OMAR aliuliza:-
Kuna wakati mwananchi anapaswa kulipa kodi zaidi ya thamani ya bidhaa au kifaa alichonacho:-
(a) Je, Serikali haioni kwamba yanapotokea hayo yanashawishi mlipa kodi husika kulipa kwa njia ya panya au kukwepa kodi?
(b) Je, ni kiasi gani cha misamaha ya kodi kimekuwa kikitolewa na Serikali kwa kipindi cha miaka kumi nyuma na ni nini athari zake katika uchumi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Hamad Omar, Mbunge wa Ole, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi kuu zinazotozwa kwenye bidhaa zinazoingizwa kutoka nje ya nchi ni Kodi ya Ongezeko la Thamani yaani VAT, Ushuru wa Bidhaa na Ushuru wa Forodha. Kiwango cha Kodi ya VAT kwa bidhaa zote zinazostahili kulipiwa VAT ni asilimia 18 bila kujali kuwa bidhaa imeagizwa kutoka nje ya nchi au imezalishwa hapa nchini. Aidha, viwango vya ushuru wa bidhaa kwa bidhaa nyingi, isipokuwa magari, hutumia viwango maalum (specific rate) kulingana na aina ya bidhaa. Kwa mfano, bia hutozwa Sh.729 kwa lita, mafuta ya petroli Sh.339 kwa kila lita na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango vya Ushuru wa Forodha vinavyotumika hapa nchini ni vile vya ushuru wa pamoja wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Ushuru huu unatumia viwango vinavyozingatia kiwango cha uchakatwaji wa bidhaa husika. Bidhaa za mtaji na baadhi ya malighafi hutozwa ushuru wa asilimia sifuri, bidhaa zilizochakatwa kwa kiwango cha kati na vipuri hutozwa asilimia 10 na bidhaa za mlaji hutozwa asilimia 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo, mfumo wa kodi kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchini unazingatia Sheria ya VAT na Sheria ya Ushuru wa Pamoja wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa minajili ya kulinda mazingira pamoja na viwanda vya ndani, kuna baadhi ya bidhaa ambazo zinatozwa Ushuru wa Bidhaa kwa zaidi ya asilimia 25. Mfano, sukari asilimia 100 au Dola za Marekani 460 kwa tani moja kwa kutumia kiwango chochote kilicho kikubwa zaidi na magari yaliyotumika kwa zaidi ya miaka kumi tangu tarehe ya kutengenezwa hutozwa ushuru wa ziada wa uchakavu wa asilimia 30.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, ni kweli kuwa kuna baadhi ya bidhaa ambazo zinaweza kutozwa kodi zaidi ya bei ya kununulia ikiwa zitaangukia katika kundi hili la kulinda mazingira pamoja na viwanda vya ndani. Aidha, ukwepaji kodi unaofanywa na baadhi ya waagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi unatokana na tabia ya waagizaji wenyewe kukosa uzalendo na si vinginevyo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi cha msamaha wa kodi uliotolewa na Serikali katika kipindi cha miaka kumi iliyopita ni shilingi trilioni 11.8 ikiwa ni wastani wa shilingi trilioni kwa mwaka.