Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Additional Answers from Prime Minister to Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani (3 total)

MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya wakazi wa Wilaya ya Malinyi, Wilaya ya Ulanga na Kilombero, tunaishukuru Serikali na tunawapa pongezi kutekeleza ahadi ambayo wametuahidi ya ujenzi wa daraja la Kilombero ambayo imekuwa jawabu kubwa la kero ya miundombinu katika Wilaya hizo tatu. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, ujenzi huo wa daraja la Kilombero unahusisha pia na barabara za maingilio na barabara hiyo ya maingilio inaunganisha barabara inayotoka Ifakara, Lupilo, Malinyi, Kilosa Mpepo, Londo, Lumecha, Namtumbo mpaka Songea. Barabara hii kipindi cha masika inachafuka sana kutegemea na mazingira ya mvua maeneo yale na inakuwa inapitika kwa tabu sana. Sasa, je, Serikali inajipangaje na ukarabati wa kudumu wa maeneo korofi katika barabara hiyo niliyotaja?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; barabara hii niliyotaja inajulikana kwa T16, barabara hiyo iko katika upembuzi yakinifu unaosanifu kwa kina ambao umekamilika. Barabara inatakiwa ijengwe kwa kiwango cha lami. Ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara hiyo inayotoka Ifakara, inatobokea mpaka Songea ambayo itakuwa sio kwa ajili ya mkaazi wa Morogoro itasaidia pia na ndugu zetu majirani wa Mkoa wa Ruvuma na Mkoa wa Njombe?
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, napokea kwa niaba ya Serikali pongezi alizotupa na kwa kweli ni wajibu wetu kutekeleza ahadi zote ambazo tumezitoa katika Ilani ya Uchaguzi ya 2015/2020.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoongelea nayo iko katika Ilani ya Uchaguzi ya 2015 hadi 2020 ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Upembuzi na usanifu wa kina haujakamilika – physically umekamilika lakini taarifa bado haijakamilika na tunatarajia hiyo kazi itakamilika mwezi Mei, 2017. Kwa sasa taarifa ya rasimu imeshawasilishwa TANROADS wanaipitia kwa kina ili hatimaye wamrudishie maoni yule Mhandisi Mshauri ambaye ni kampuni ya Kyong Dong na baada ya hapo ndio atakuja kukamilisha kuandika taarifa ya mwisho. Kwa ratiba ilivyo ataiwasilisha taarifa ya mwisho mwezi Mei, 2017. Baada ya hapo Serikali itaanza kujipanga kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la ukarabati wa maeneo korofi kwa sasa ili iweze kupitika muda wote; nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Hadji Mponda Mbunge wa Malinyi na wananchi wote wa Malinyi hadi Kilosa kwa Mpepo kwamba Serikali ina mkakati kabambe na kila mwaka tunatenga fedha na nafahamu mwaka huu kuna wakandarasi wawili wako site katika maeneo korofi wanafanyia ukarabati wa hali ya juu ili kuhakikisha barabara hiyo inapitika mwaka mzima bila matatizo.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kukamilika kwa daraja la Mto Kilombero ni wazi kwamba sasa Mkoa wa Morogoro unafunguliwa kibiashara. Nini mipango ya Serikali kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Lindi kwa barabara inayopitia kutoka Liwale kuelekea Morogoro? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kiongozi wetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikuwa ni moja kati ya ahadi yake ya kuhakikisha barabara kutoka Ilonga hadi Liwale inashughulikiwa. Ahadi hiyo tumepewa na nimhakikishie kwamba tutaishughulikia hadi tuikamilishe katika kipindi hiki cha miaka mitano.
MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali juu ya ujenzi wa daraja la Kilombero lakini ahadi ya Serikali ya kukamilisha ujenzi wa barabara kupitia daraja la Kilombero kwenda Songea kupitia Namtumbo ni ya muda mrefu sana na hivi sasa wananchi wa Songea ukitaka kusafiri kwa kawaida ni masaa 15 kutoka Dar es Salaam mpaka Songea. Hii barabara kutoka Kilombero kukatiza Namtumbo kwenda Songea ingerahisisha sana na usafiri ungekuwa mwepesi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni vizuri Serikali itupe majibu ni lini tunatazamia tuanze ujenzi wa barabara hii ya kuelekea Songea kupitia Kilombero? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli hoja ya kujenga barabara hii ilianza toka mwaka 1996, tunafahamu. Tatizo lililokuwepo katika kipindi kirefu sana tulikosa fedha lakini hatimaye katika kipindi hiki na Serikali hii ya Awamu ya Tano naomba nimhakikishie kwamba kazi hii itafanyika muda si mrefu na kwa vyovyote ni ndani ya kipindi cha miaka mitano ambayo ahadi imetolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anafahamu, akiangalia kitabu chetu cha Ilani atakuta hii barabara imeandikwa itajengwa kwa kiwango cha lami na hatua za mwanzo ndio hivyo tunazikamilisha mwezi Mei na baada ya hapo tunaanza utaratibu wa kutafuta fedha za kujenga hiyo barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine vile vile mimi mwenyewe natoka Namtumbo na nimetoa ahadi kwamba barabara hii mwaka huu lazima itoboke, isipotoboka TANROADS watatoboka! Kwa hiyo, nimhakikishie suala la kutoboa barabara hii, itatoboka mwaka huu, lakini kuanza ujenzi ni baada ya miaka ijayo ya fedha.