Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Eng. Stella Martin Manyanya (1 total)

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Serikali imekuwa ikiwekeza fedha nyingi katika miradi ya ujenzi wa meli katika maziwa makubwa yaliyoko nchini mwetu likiwemo Ziwa Viktoria, Nyasa na sasa Tanganyika. Hata hivyo kumekuwa na ufanisi mdogo sana katika kutoa huduma kutumia meli hizo katika maziwa hayo:-

Je, ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kuwa meli hizi zilizojengwa kwa gharama kubwa zinatumika ipasavyo ikiwemo katika Ziwa Nyasa?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eng. Stella Manyanya, Mbunge wa Mbambabay, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeimarisha sana huduma za usafiri kwenye kada zote, maeneo yote ya barabara, hewani, kwenye maji, lakini pia kwa njia ya reli. Kama ambavyo Watanzania mnajua, miradi kadhaa inaendelea ikiwemo na utengenezaji wa meli ambazo zinatoa huduma kwenye maziwa yetu na ukanda wa bahari ikiwemo na Ziwa Nyasa; na kwa bahati nzuri nimepata nafasi ya kwenda Nyasa na kuzindua meli kadhaa: -

Mheshimiwa Spika, sasa Mheshimiwa Mbunge anaomba kujua utoaji huduma wenye tija; ni swali pana kidogo.

Mheshimiwa Spika, utoaji huduma wenye tija, mkakati wetu ndani ya Serikali, kwanza ni kupanua wigo wa kufanya biashara hiyo na kwa kuwahudumia Watanzania. Hii ina maana ya kwamba, kama tuna vituo vichache vinavyolazimisha wananchi walioko mbali kufuata bandari, lakini kwenye maeneo walimo, tunaweza kujenga bandari. Ndiyo mkakati ambao sasa unafanywa na Mamlaka ya Bandari kwa kujenga bandari palipo na watu wengi ili kuweza kuwafikia ili huduma sasa iwe na tija. Hiyo ni moja.

Mheshimiwa Spika, pili, sisi tunafanya kazi kule Ziwa Nyasa na nchi ya Malawi. Nchi ya Malawi ni ndefu kufuata lile ziwa, lakini tuna bandari moja tu ya upande wa Malawi. Sasa ili kufanya huduma hizi ziwe zenye tija, nako pia kushawishi kuwa na bandari nyingine ili tuweze kuwapata abiria wengi ili na yenyewe iweze kuwafikia Watanzania kwenye huduma hii.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tunataka tuimarishe ratiba za meli ziwe mara nyingi zaidi kuliko ratiba ambayo inawafikia wananchi mara chache. Labda kama ratiba hiyo ni mara moja kwa wiki, basi tupeleke mpaka mara mbili, mara tatu, zipite, wananchi wafanye maamuzi ya kufanya biashara yao kwa urahisi zaidi. Hiyo nayo pia inaingia kwenye tija aliyoisema Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, pia, kwa tukio ambalo limetokea kule Nyasa siku za karibuni, meli zetu ziliharibika kwa muda mrefu. Nayo pia inaweza kuwa siyo tija. Nataka niwahakikishie, tumeimarisha ukarabati wa hizi meli. Nimeenda Kyela, nimekuta meli zetu, tukaagiza wale watendaji wa TASAC waikamilishe kusimamia ukarabati wa zile meli na zianze mara moja. Taarifa ambayo tumezipata, meli zimeshaanza kufanya kazi. Kwa hiyo, nayo pia inaleta tija katika utoaji huduma kwenye ukanda wetu. Kwa kufanya hilo tutaimarisha pia ukaguzi wa mara kwa mara, ili meli zisisimame wananchi waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, vile vile tunapunguza gharama za kuingia na kusafiri na kusafirisha mizigo ili kuvutia watu wengi zaidi kutumia meli hizo. Nadhani huo ndiyo mkakati ambao tunaufanya ndani ya Serikali ili kuleta tija kwa Watanzania ambao tumekusudia kuwahudumia.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Nyasa, pia tuna Mbunge hapa wa Kyela, tuna Mbunge hapa wa Ludewa, maeneo yote haya yananufaika na meli yetu kwenye Ukanda ule wa Ziwa Nyasa. Niwahakikishie Serikali itaendelea kutoa huduma kwenye maeneo hayo. Ahsante sana. (Makofi)