Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha (17 total)

MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Miaka kadhaa iliyopita Serikali iliahidi kuwa itajenga barabara ya kutoka Kitai Wilayani Mbinga hadi Lituhi Wilayani Nyasa kwa kiwango cha lami, lakini hadi sasa wananchi hawaelewi kinachoendelea juu ya ujenzi huo:-
Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Mbinga na Nyasa juu ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Kitai - Lituhi yenye urefu wa kilometa 84.5 ni barabara ya mkoa inayohudumiwa na Wakala wa Barabara Mkoa wa Ruvuma. Ili kuhakikisha kuwa barabara hii inapitika muda wote, Wizara inaendelea kutenga fedha za kufanyia matengenezo mbalimbali ambapo mwaka 2013/2014 ilitenga shilingi milioni 440 na mwaka 2014/2015 ilitenga shilingi 682.99. Katika mwaka wa fedha 2015/2016, jumla ya shilingi milioni 1015.123 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hii ili iendelee kupitika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maandalizi ya ujenzi wa barabara za Kitai - Lituhi kwa kiwango cha lami, Wizara kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) tayari imekamilisha taratibu za ununuzi za kumpata Mhandisi Mshauri kwa ajili ya kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara hiyo.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Wananchi wa Tarafa za Hagati, Mbuji na Mkumbi hawapati matangazo ya Redio ya TBC kutokana na Kituo cha TBC- Songea kutokuwa na uwezo wa kurusha matangazo na badala yake wanapata matangazo ya redio toka nchi jirani ya Malawi:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza uwezo wa kurusha matangazo ya kituo cha TBC- Songea ili wananchi wa Tarafa hizo wapate habari kupitia TBC?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, matangazo ya Radio ya Taifa kupitia mtambo wa masafa ya kati yaani Medium Wave yenye nguvu ya Kilowati 100 yalikuwa yakisikika vizuri katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma wakati mtambo huo ulipokuwa ukifanya kazi. Tangu mwezi Julai, 2013 mtambo huo haufanyi kazi kutokana na uchakavu na hivyo kuathiri usikivu wa matangazo ya TBC katika maeneo kadhaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa wananchi kupata matangazo, TBC ililazimika kuhamisha mitambo yake miwili ya Radio yenye uwezo wa Kilowati moja kwa kila mmoja iliyokuwa imefungwa eneo la Mshangano - Songea na kuifunga eneo la juu la mlima wa Matogoro (Songea) ili angalau usikivu wake usambae eneo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kufunga mitambo hiyo, matangazo ya TBC- Songea yameboreshwa. Hata hivyo, kutokana na uwezo mdogo wa mitambo ya FM inayotumika kwa sasa mawimbi yake ya sauti hayafiki mbali sana ukilinganisha na yale ya mitambo ya Medium Wave iliyokuwa ikitumika wakati wa awali ambayo yanafika eneo kubwa zaidi la Mkoa wa Ruvuma zikiwemo Tarafa za Hagati, Mbuji, na Mkumbi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kukabiliana na changamoto za usikivu hafifu katika maeneo kadhaa Mkoani Ruvuma, TBC imeshafanya upembuzi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM yenye uwezo wa kilowati moja katika eneo la Mbamba Bay lililopo Wilaya ya Nyasa ili kuongeza usikivu wa redio na TBC. Katika bajeti ya mwaka wa 2016/2017, Wizara yangu imetenga fedha za maendeleo kwa ajili ya kufunga mtambo eneo la Mbamba Bay. Kazi hiyo ya uboreshaji wa matangazo katika eneo hilo itaanza mara tu fedha za kununua na kufunga mitambo zitakapotolewa.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Wilaya ya Mbinga imebahatika kupata mradi wa kujenga barabara ya lami toka Kijiji cha Longa hadi Kijiji cha Litoha kwa kiwango cha lami kwa ufadhili wa Umoja wa Nchi za Ulaya na mradi huo umeshaanza kutekelezwa:-
(a) Je, ujenzi wa mradi huo unategemewa kukamilika lini?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalipa fidia wananchi waliotoa mashamba na nyumba zao kupisha ujenzi wa mradi huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba wa ujenzi wa barabara awamu ya kwanza kutoka Longa hadi Bagamoyo ulianza tarehe 1/10/2015 na unategemewa kukamilika tarehe 30/6/2016. Hata hivyo, kutokana na mvua kubwa zilizonyesha Wilaya ya Mbinga, Mkandarasi alishindwa kufanya kazi kama ilivyokuwa imepangwa hali iliyolazimu kuongeza muda hadi tarehe 30/9/2016. Sehemu ya pili inaanzia Kijiji cha Bagamoyo hadi Kijiji cha Lutoho chini ya Mkandarasi GS Contractors Limited ambaye mkataba wake ulianza tarehe 1/5/2016 na unategemewa kumalizika tarehe 30/1/2017.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, sharti lilitolewa na Umoja wa Ulaya ili waweze kujengewa barabara ya lami kutoka Longa hadi Bagamoyo lilikuwa ni kutokuwepo kwa fidia. Halmashauri kwa maana ya Madiwani walifanya uhamasishaji wa kutoa elimu kwa wananchi ili kukubali mradi huo na wote waliridhia ndiyo maana barabara hiyo imeanza kujengwa. Serikali inawapongeza viongozi wa Halmashauri na wananchi kwa ujumla kwa kukubali kuupokea mradi huo kwa ustawi wa uchumi wa maendeleo ambayo ni uzalishaji mkubwa wa kahawa.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Wananchi wa Mbinga wanaishukuru Serikali kwa mradi wa kusambaza umeme vijijini kwani wana imani mradi huo utasaidia kuinua hali za maisha. Hata hivyo ni vijiji 34 tu ndiyo vimepatiwa umeme kupitia mpango wa usambazaji umeme unaotekelezwa na REA Awamu ya Pili.
Je, lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 118 vilivyosailia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini napenda sasa kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alezander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka umeme katika vijiji 118 vilivyobaki vya Wilaya ya Mbinga kupitia mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu. Ujenzi wa mradi huu utaanza mwezi Disemba, 2016 na kukamili katika kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020. Hatua iliyofikiwa hivi sasa ni kukamilika kwa taratibu za kuwapata wakandarasi watakaohusika na ujenzi wa mradi huu.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovolti 0.4 yenye urefu wa kilometa 471, ufungaji wa transfoma 246 pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 19,185. Kazi hii itagharimu shilingi bilioni 18.1.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Katika msimu wa kilimo wa mwaka 2015/2016 Mawakala wa Usambazaji Pembejeo kwa Vocha katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga wanaidai Serikali jumla ya Sh.824, 000,000/=
Je, Serikali ina mpango gani wa kulipa deni hilo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu wa kilimo wa mwaka 2015/2016, Serikali ilitoa ruzuku ya pembejeo kwa utaratibu wa vocha kwa mikoa 25 ya Tanzania Bara. Kazi ya kusambaza pembejeo hizo kwa kaya za wakulima wanufaika wapatao 999,926 ilifanywa na makampuni na Mawakala wa Pembejeo katika Halmashauri zipatazo 144 zilizonufaika na utaratibu huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kujiridhisha na uhalali wa madai ya makampuni ya Mawakala waliotoa huduma ya pembejeo katika Wilaya hizo, Wizara imefanya uhakiki wa awali ambao umefanyika katika baadhi ya mikoa yenye kiasi kikubwa cha madai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya uhakiki wa awali imefanyika katika mikoa nane kati ya mikoa 25 ya Tanzania Bara iliyopata ruzuku. Matokeo hayo yameonesha upungufu mkubwa katika madai hayo. Hivyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Fedha na Mipango kufanya uhakiki katika mikoa yote kwa makampuni na Mawakala wote waliosambaza pembejeo katika msimu wa 2015/2016 katika kipindi cha mwezi mmoja. Baada ya uhakiki huo madeni yote halali yatalipwa.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
(a) Je, kuna vituo vingapi vinavyorusha matangazo kwa njia ya televisheni nchini na vinamilikiwa na Kampuni zipi?
(b) Je, ni vituo vingapi vinarusha matangazo ya televisheni bure kwa wananchi kupitia ving’amuzi?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO, alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya mawasiliano Tanzania imetoa leseni kwa vituo 32 vya Television hapa nchini. Orodha ya vituo hivyo na wamiliki wa vituo hivyo ni ndefu naomba nisiisome hapa ila nimekwishamkabidhi Mheshimiwa Mbunge na ninaomba iingie kwenye Hansard.
(b)Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania hutoa leseni ya maudhui ya utangazaji wa televisheni za aina mbili. Leseni za maudhui yanayotazamwa bila kulipia (free to air) na maudhui ya kulipia (pay tv). Aidha, leseni hizi zimegawanywa kimasoko. Kuna leseni za kitaifa ambazo hupaswa kuonekana nchi nzima na kuna leseni za kimkoa ambazo huruhusiwa kutangaza mikoa kumi ya Tanzania Bara na leseni za kiwilaya ambazo huonekana mkoa mmoja.
Mgawanyo huu wa kimasoko unatoa fursa kwa waombaji kutangaza maeneo wanayochangua kutokana na uwezo wao wa kifedha na na kiuendeshaji. Maudhui haya ya bila kulipia huonekana kupitia ving’amuzi vya Mkampuni ya Agape Associates Limited, Basic Transmission Limited na Star Media Tanzania Limited. Visimbuzi hivi ni TING, Startimes, DIGITEC na CONTINENTAL Vituo vyenye leseni ya soko la kitaifa ni TBC1, Channel 10, East Africa Televison, Independent Television, Star Television, Clouds TV na Bunge TV. Vituo vyenye soko la kimkoa ni TV Imaan, Agape TV (ATV) na TV1 zilizobaki zina soko la kiwilaya.
Aidha, Kituo cha TBC1 ambacho ni kituo cha umma (public broadcaster) kinapatikana bila malipo ya mwezi kwenye ving’amuzi vyote vya miundombinu isiyosimikwa ardhini yaani Digital Terrestrial Television na vile vinavyotumia mitambo ya satelite yaani direct to home kama vile Azam TV, DSTV na Zuku. Kituo cha TBC1 kinalazimika kuonekana bila malipo kwa mujibu wa masharti ya leseni za makampuni ya miundombinu ya utangazaji wa ardhini yaani DTT na Satelite (DTH).

ORODHA YA VITUO VYA TELEVISHENI NA WAMILIKI WAKE

1. Independent Television (ITV) - Reginald Mengi & Family Trust 99% & Reginald Abraham Mengi 1%
2. Star Television - Diallo Investment Co. Limited 50% & Nyalla Investment Co. Limited 50%
3. Channel Ten Television - Africa Media Group Limited 100%
4. TBC 1 - Tanzania Broadcasting Corporation 100%
5. TBC 2 - Tanzania Broadcasting Corporation 100%
6. East Africa Television (EATV) - Reginald Mengi & Family Trust 99% & Reginald Abraham Mengi 1%
7. Agape Television (ATV) - World Agape Ministries 100%
8. C2C Television - Africa Media Group Limited 100%
9. Dar es Salaam Television (DTV) - Africa Media Group Limited 100%
10. Abood Television - Aziz Mohammed Abood 50% & Fauzi Mohammed Abood 50%
11. CTN Television - Africa Media Group Limited 100%
12. Capital Television - Reginald Mengi & Family Trust 99% & Reginald Abraham Mengi 1%
13. Clouds TV - Joseph Mlebya Kusaga 50%, Andrew Dogan Kusaga 20% & Alex Kusaga Mkama 30%
14. VIASAT 1 Television - Dr. Gideon H. Kaunda 7.5%, Ambassador Paul Milyango Rupia 7.5% & Dr. Wilbert Basilius Kapinga 36%
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Kwa takwimu za miaka ya hivi karibuni uzalishaji wa kahawa Wilayani Mbinga umeonekana kushuka kwa mkulima mmoja mmoja (out growers). Na sababu mojawapo ya kushuka kwa uzalishaji huo ni kuzeeka kwa miti ya kahawa.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapelekea wakulima wa Mbinga mbegu mpya ili kuinua uzalishaji?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka mnada wa kahawa Wilayani Mbinga, badala ya minada hiyo kuendelea kufanyika Moshi?
(c) Je, Serikali ina mkakati gani wa kupiga marufuku kabisa uuzaji wa kahawa mbichi ikiwa shambani, maarufu kama “magoma” Wilayani Mbinga?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Msuha, Mbunge wa Mbinga, swali lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali wa kuwapelekea wakulima wa Mbinga mbegu mpya ili kuinua uzalishaji ni kwa kutekeleza mpango mkakati wa kuendeleza zao la kahawa kwa miaka kumi (2011 – 2021). Katika mpango huo utafiti na usambazaji wa miche bora, ili kuondokana na miche yenye tija duni na iliyo zeeka ni mojawapo ya kipaumbele. Utekelezaji wake unafanyika kwa kushirikiana na wadau, hususan Tanzania Coffee Research Institute (TaCRI). Kituo cha utafiti na uzalishaji miche cha Ugano kilichoko Wilayani Mbinga katika mwaka 2016/2017 kilizalisha na kusambaza miche bora ya kahawa 270,869 na kazi inaendelea. Aidha, Mfuko wa Maendeleo ya Kahawa (Tanzania Coffee Development Fund) umefadhili na kupunguza bei kutoka shilingi 300 kwa mche mmoja hadi shilingi 150 kwa vituo vyote nchini vilivyoko chini ya TaCRI ili miche hiyo isambae kwa kasi.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mnada wa kahawa huendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Kahawa Namba 23 ya mwaka 2001. Serikali haina mpango wa kuanzisha Soko la Mnada wa Kahawa - Mbinga au mahali pengine nchini kwa sababu, uwepo wa miundombinu ya mashine ya kielektroniki ya kuendesha mnada iliyopo Moshi, maabara ya kuonjea kahawa, wataalam wa kuendesha mnada hu, gharama za mnunuzi ambapo atalazimika kwenda katika kila mnada, kama utawekwa kila mahali ambapo kahawa inazalishwa uzoefu unaonesha kuwa nchi nyingi duniani huweka mnada sehemu moja tu, ili kurahisisha uendeshaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tangu kuanzishwa kwake kabla ya uhuru mnada uliwekwa Moshi kwa kuwa ndiko kulikua na wanunuzi na biashara ukilinganisha na maeneo kama Kagera, ingawa uzalishaji unafikia hadi asilimia 40 ya nchi nzima. Mnada unauza kahawa ikiwa kwenye maeneo ya uzalishaji kwa mfano kule Mbinga na Mbeya, n.k. KInachopelekwa Moshi ni sampuli tu kwa ajili ya uonjaji.
Aidha, Serikali imeanzisha soko la bidhaa (Commodity Exchange) ili kupunguza gharama za uendeshaji wa masoko ya mazao ikiwemo kahawa.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kifungu Namba 29(ii) cha Kanuni za Kahawa 2013, ni kosa kwa mtu yeyote kununua matunda ya kahawa (ripe cherry) kwa hiyo, Serikali inakataza biashara ya kahawa mbichi. Naomba nitoe agizo kwa Mkuu wa Wilaya ya Mbinga na Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla, wote kwa pamoja na wahusika wengine wote kwamba, hairuhusiwi kabisa uuzaji wa kahawa mbichi.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Chama Kikuu cha Ushirika ‘Mbinga Cooperative Union (MBICU) kilishindwa kuendesha shughuli zake kibiashara na hatimaye kukabidhiwa kwa mfilisi mwaka 1994/1995 kutokana na madeni pamoja na kuyumba kwa soko la kahawa.
(a) Je, kwa nini mfilisi bado anashikilia mali za Chama hicho badala ya kukabidhi kwa Chama kipya cha Mbinga Farmers Cooperation Union (MBIFACU) kwa muda mrefu kiasi hicho?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kulipa deni la wakulima lipatalo shilingi 424 millioni ambalo liliachwa na MBICU iliyokufa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, lenye sehemu (a)na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Chama Kikuu cha Ushirika cha Mbinga (MBICU Limited) kiliacha shughuli zake baada ya kuelemewa na madeni na hivyo kusababisha kufutwa kwenye daftari la Serikali na kisha kufilisiwa. Sababu kubwa na ya msingi ya kufilisiwa MBICU Limited ni kudaiwa na Benki ya NBC na wadai wengine kiasi cha Sh.2,101,365,050/= ambapo ilijikuta ni mufilisi kwa kuwa mali zake zilikuwa na thamani ya Sh.752,814,784/=.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Mfilisi hajashikilia mali zozote za MBICU Limited, baada ya kufutwa kwa MBICU Limited wanachama walianzisha MBIFACU Limited kwa mategemeo ya kukabidhiwa mali za MBICU Limited. Mwaka 2007, wanachama walianzisha MBIFACU Limited, walirudishiwa mali zao na kuahidi kulipa madeni yanayodaiwa MBICU Limited likiwepo deni la Golden Impex Limited lililokuwa na thamani ya Sh.155,000,000/= ambalo lililipwa tarehe 13 Machi, 2012.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya deni hilo kulipwa MBIFACU Limited ilikabidhiwa asilimia sabini ya mali na mfilisi na Bodi ya Uongozi wa MBIFACU Limited ilianza kusimamia mali hizo. Sehemu ya mali ya asilimia 30 iliyobaki itakabidhiwa baada ya Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika kujiridhisha na utekelezwaji wa Mkataba wa Maridhiano yaani MoU baina ya Mfilisi na MBIFACU Limited.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya mipaka ya baadhi ya maeneo kama vile mikoa, wilaya na majimbo ya uchaguzi kwani baadhi ya mipaka ya maeneo hayo yana muingiliano unaoleta ugumu wa utoaji wa huduma za jamii?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuligawa Jimbo la Mbinga Vijijini kwa kuzingatia ukubwa wake wa kata 29?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kufanya mapitio ya mipaka kwa baadhi ya mikoa, wilaya na majimbo ya uchaguzi hasa yenye muingiliano unaosababisha ugumu wa utoaji wa huduma za jamii. Hata hivyo, zoezi hilo ambalo linaweza kusababisha mapendekezo ya maeneo mapya ya utawala au kuyahamisha mengine litafanyika baada ya kukamilisha miundombinu ya majengo ya ofisi, majengo ya huduma mbalimbali na vifaa katika mikoa, wilaya na halmashauri mpya zilizoanzishwa tangu mwaka 2012.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imepewa mamlaka ya kuyagawa majimbo ya uchaguzi kwa kuzingatia vigezo vya idadi ya watu, jiografia, hali ya mawasiliano, ukubwa wa jimbo na uwezo wa ukumbi wa Bunge. Ili jimbo ligawanywe Tume hutoa tangazo kuhusu nia hiyo. Baada ya tangazo, mapendekezo hujadiliwa katika vikao vya halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa na hatimaye huwasilishwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo hutangaza Jimbo jipya baada ya kupata kibali cha Rais.
MHE. MARTIN A. M. MSUHA aliuliza:-
Je, ujenzi wa barabara ya Mbinga hadi Mbambabay kwa kiwango cha lami unatarajiwa kukamilika lini?
NAIBU WAZIRI UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO – (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Msuha Mbunge wa Mbinga Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya Mbinga Mbambabay yenye urefu wa kilometa 66 umeanza ambapo tarehe 3, Aprili, 2018 Wizara yangu kupitia Wakala wa barabara Tanzania TANROADS ilisaini mkataba wa ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara hii na kampuni ya China Henan International Corporation group company limited (CHICO) ya nchini China kwa gharama ya Sh,129,361,352,517.84 na muda wa ujenzi wa miezi 33 hadi tarehe 2 Januari, 2021.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya ujenzi inasimamiwa na mwandishi mshauri SMES International Limited wa nchini Australia kwa gharama ya Dola za Kimarekani 1,818,649.42 na fedha za kitanzania Sh.7,179,356,000.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Je, Serikali itakamilisha lini mradi wa kusambaza maji kwa wananchi waliopo pembezoni mwa bomba kuu litokalo Ruvu Juu hadi Dar es Salaam hususan wananchi wa Kata za Kwembe, Mbezi, Kibamba, Msigani na Saranga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Msuha, Mbunge wa Mbinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali imemwajiri mkandarasi Kampuni ya Jain Irrigation Services kutekeleza mradi wa usambazaji maji kwa wananchi waishio maeneo ya pembezoni mwa bomba kuu litokalo Ruvu Juu hadi Dar Salaam hususani wananchi wa Kata za Kwembe, Mbezi, Msigani na Saranga.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Mei, 2018, utekelezaji wa mradi huo ulikuwa umekamilika kwa wastani wa asilimia 87. Kazi inayoendelea kwa sasa ni kukamilisha ulazaji wa mabomba na kufanya majaribio (Pressure test). Mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2018. (Makofi)
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itafanya utafiti wa gharama za uzalishaji wa kahawa Wilayani Mbinga kwa mara ya mwisho?

(b) Je, utafiti huo ulibaini kilo moja ya kahawa kavu inazalishwa kwa gharama gani?

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Mtonda Msuha, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2015/ 2016, Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kahawa Tanzania (TACRI) imefanya utafiti wa gharama za uzalishaji wa kahawa katika Wilaya saba za Mbinga, Mbozi, Tarime, Rombo, Muleba, Karagwe na Buhigwe ambazo ni miongoni mwa Wilaya zinazozalisha zao la kahawa hapa Nchini.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti uliofanywa na Kituo cha Utafiti cha TACRI kwa wakulima wa kahawa aina ya arabica umeonesha kuwa gharama za uzalishaji wa aina bora ya kahawa zenye ukinzani wa magonjwa ni shilingi Sh.2,192,000 kwa hekta sawa na wastani wa Sh.825.44 kwa kilo zenye tija ya wastani wa kilo 2,662 kwa hekta. Aidha, gharama za uzalishaji wa kahawa zisizo na ukinzani wa magonjwa ni Sh.2,571,200 kwa hekta sawa na wastani wa kilo 1,931.78 kwa kilo zenye tija za wastani wa kilo 1.331 kwa hekta. Aidha, gharama za uzalishaji wa kahawa wa aina hiyo zimeongezeka kutokana na matumizi makubwa ya viuatilifu vya kuzuia kutu ya majani (Coffee Leaf Rust) na Chulebuni ambayo Coffee berry disease yaani CBD.

Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti pia umeonesha, wakulima wanaolima kilimo cha mseto yaani intercropping kwa kuchanganya zao la kahawa na migomba, gharama za uzalishaji ni wastani wa Sh.1,557,683 kwa hekta kwa kahawa bora na Sh.2,157,967 kwa kahawa isiyo na ukinzani kwa magonjwa. Aidha, kupitia tafiti hizo, Serikali imekuwa ikishauri wakulima kutumia aina bora za kahawa ili kuwa na kilimo chenye tija, faida na endelevu.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-

Hivi karibuni Serikali ilibadilisha mfumo wa ununuzi na uuzaji kahawa kwamba ni lazima kupitia Vyama vya Ushirika vya Msingi:-

Je, ni Vyama vingapi vya Msingi vya Ushirika (AMCOs) vimeundwa Wilayani Mbinga kufuatia kubadilishwa kwa mfumo huo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Martin Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, naomba kutoa maelezo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vyama vya Ushirika huanzishwa na wananchi kutokana na mahitaji yao, hivyo, kupelekea kuwepo kwa aina mbalimbali za Vyama vya Ushirika kama vile vyama vya ushirika vya mazao ya kilimo na masoko, mifugo, uvuvi, viwanda, nyumba, fedha na madini kwa mujibu wa Sheria ya Ushirika Na. 6 ya mwaka 2013.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali imeelekeza biashara ya zao la kahawa na mazao mengine ya biashara kufanyika kupitia Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) badala ya wanunuzi binafsi kwenda kwa wakulima moja kwa moja. Utaratibu huu utawawezesha wakulima kunufaika na kilimo cha kahawa kwa kuzalisha kahawa yenye ubora na kuzwa kupitia minada ambapo wanunuzi watashindanishwa na hivyo kupelekea mkulima kupata bei nzuri na yenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi sasa Mkoa wa Ruvuma una jumla ya Vyama vya Ushirika vya Msingi vya Kahawa 67 na Chama Kikuu cha Ushirika kimoja (MBIFACU) ambavyo vimeansihwa na wakulima wa kahawa katika Mkoa wa Ruvuma. Aidha, Wilaya ya Mbinga ina jumla ya Vyama vya Ushirika vya Msingi vya Kahawa 58 ambavyo ndivyo vitasimamia na kuendesha biashara ya kahawa katika Wilaya ya Mbinga.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha Sheria ya Vyama vya Ushirika ili kuondoa upungufu uliopo, hususan kwenye upande wa Uanachama na kuipa Serikali nguvu za Kisheria juu ya Vyama vya Ushirika?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Msuha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa sote tunaelewa kuwa ushirika ni dhana ya hiari, lakini Serikali ni msimamizi mkuu wa vyama vya ushirika pale ambapo viongozi wake au vyama vyenyewe havitekelezi malengo yaliyokusudiwa na ushirika. Serikali inakiri vyama vinakabiliwa na changamoto za kiutendaji, usimamizi, viongozi kutokuwa waadilifu na upungufu wa kimfumo wa uendeshaji wa baadhi ya Vyama vya Ushirika hapa nchini. Hata hivyo, vipo baadhi ya Vyama vya Ushirika ambavyo vinafanya vizuri, mfano, Chama cha Ushirika cha Chai kilichopo Wilaya ya Mafinga kinachoitwa Chamkonge na Chama cha Ushirika cha Kahama (KACU).

Mheshimiwa Naibu Spika, ushirika ndicho chombo cha kuwaletea wananchi maendeleo ya kiuchumi kwa kuwaunganisha wakulima ili kuwa na nguvu ya pamoja katika kutoa huduma za ugani, upatikanaji wa pembejeo na kutafuta masoko ya mazao. Aidha, Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi 2015 – 2020 Ibara ya 22(g) na 86(a) inaelekeza kuifanyia mapitio Sera ya Vyama vya Ushirika na kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Vyama vya Ushirika na upatikanaji wa takwimu zitakazosaidia kuandaa mipango na kuleta mageuzi katika sekta ya ushirika na kuimarisha uchumi wa taifa na kuviimarisha vyama vya ushirika kuwa na uwezo wa kutafuta masoko ya mazao ya wakulima ya ndani na nje kwa kuweka mfumo madhubuti wa ukusanyaji, uchambuzi na uenezaji wa taarifa za masoko na kutoa elimu juu ya uongezaji thamani na biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Kilimo ipo katika hatua za mwisho kuleta Bungeni mapendekezo ya mabadiliko ya Sheria ya Maendeleo ya Ushirika yatakayoendana na mahitaji ya sasa ambayo yatahusisha mabadiliko ya mfumo na muundo wa uongozi ili kuendana na mahitaji ya teknolojia na kuleta ushindani wa kibiashara.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-

Tangu uhuru Wilaya ya Mbinga imekuwa ikitegemea zao moja la biashara ambalo ni kahawa:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka zao lingine la biashara Wilayani humo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya utafiti wa afya na tabaka la udongo katika kanda saba za kilimo zenye kuwezesha uzalishaji wa mazao mbalimbali kulingana na ikolojia ya kanda husika. Kanda hizo za kiikolojia ni pamoja na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini inayohusisha Wilaya ya Mbinga na Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na utafiti huo, Serikali imeandaa mwongozo wa uzalishaji wa mazao kwa kuzingatia ikolojia ambapo Mkoa wa Ruvuma una fursa kubwa ya kuzalisha mazao mengine ya biashara tofauti na kahawa ikiwemo mazao ya korosho, muhogo, alizeti, ufuta na matunda yanayostawi katika ukanda wa baridi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima katika Halmashauri ya Mbinga wamehamasishwa na wameanza uzalishaji wa kibiashara wa mazao ya korosho, alizeti, ufuta, soya, parachichi, miwa, tumbaku pamoja na mazao mapya kama macadamia. Aidha, Serikali inaendelea kusimamia uendelezaji wa mazao kwa kuhamasisha matumizi ya teknolojia bora katika mnyororo wa thamani, kuongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kilimo pamoja na kuimarisha ushirika na mifumo ya masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu wa mwaka 2016/2017, Serikali kupitia Bodi ya Korosho ilitoa mafunzo ya uzalishaji wa miche bora ya korosho kwa vikundi sita vya wakulima vya Jembe Halimtupi Mtu group, Chapakazi Group, Twiga Group, Juhudi Group, Kiboko Group na Koroshomali Group ambapo kwa pamoja vilizalisha jumla ya miche bora 111,336 na kuisambaza kwa wakulima kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa zao hilo. Aidha, msimu wa mwaka 2018/2019, jumla ya hekta 29,374.6 zilipandwa mazao ya biashara katika Wilaya ya Mbinga ambapo kati ya hizo, hekta 265 zilitumika kuzalisha zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu wa 2018/2019, eneo la hekta 806 zilitumika kuzalisha zao la soya, hekta 317 zao la alizeti, hekta 240 ufuta, hekta 32 miwa na hekta 89.5 ni parachichi. Uzalishaji wa zao la soya umeongezeka kutoka tani 42.6 msimu wa mwaka 2017/2018 hadi kufikia tani 403 msimu wa mwaka 2018/2019. Aidha, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga inayo ikolojia inayoruhusu uzalishaji wa mazao mengi ya biashara, Serikali itaendelea kuimarisha huduma za ugani ili mazao hayo yazalishwe kwa wingi na tija.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA (K.n.y. MHE. MARTIN A. MSUHA) aliuliza:-

Uhaba wa walimu wa Hisabati na Sayansi umeathiri sana matokeo ya darasa la saba mwaka 2017 Wilayani Mbinga.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka walimu wa masomo hayo Wilayani Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA W. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, zipo sababu mbalimbali zilizopelekea kushuka kwa ufaulu wa wanafuzi wa darasa la saba wa mwaka 2017 Wilaya ya Mbinga ikiwemo. Upungufu wa walimu, ushiriki hafifu wa wazazi husasani kufatilia maendeleo ya watoto wao, utoro na nyingine nyingi. Walimu wa shule za msingi wanaoajiriwa wanaweza kufundisha masomo yote yaani Sanaa na Sayansi pamoja na Hisabati.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 na 2018/2019 Serikali imeajiriwa walimu 14,422 ambapo 10,695 ni walimu wa shule za msingi za 3,727 ni walimu wa shule za sekondari. Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga imepatiwa jumla ya walimu 143 kati hayo walimu 112 ni wa shule za msingi na walimu 31 ni wa shule za sekondari. Kati yao 28 ni wa Sayansi na Hisabati, mmoja masomo ya biashara na wawili ni walimu wa fasihi kiingereza (English Literature). Serikali itaendelea kuajiri walimu na kuwapanga kwenye Halmashauri hasa zenye upunugufu wa walimu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Gereza Kuu Kitai lililopo Wilaya Mbinga?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Msuha, Mbunge Wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Gereza Kuu Kitai ni miongoni mwa Magereza ya wazi lililojengwa kwa lengo la shughuli za kilimo na mifugo. Hata hivyo, Serikali inatambua tatizo la uchakavu hususani uzio wa Gereza uliozungushiwa kwa waya (Barbed Wire Fence) na nguzo za miti ambazo zimekuwa zikishambuliwa mara kwa mara na mdudu mchwa.

Mheshiwa Spika, katika kutambua tatizo la uchakavu huo, Serikali ina mpango wa kuyafanyia ukarabati mkubwa majengo na miundombinu ya magereza nchini likiwemo Gereza Kuu Kitai kwa kuzungushia Uzio kwa tofali na ukarabati wa mabweni ili kuboresha huduma za wafungwa na mahabusu.

Mheshimiwa Spika, aidha, ukarabati na uboreshaji wa miundombinu hiyo imepangwa kutekelezwa kwa awamu kwa kutegemea na upatikanaji wa rasilimali fedha.