Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Sixtus Raphael Mapunda (9 total)

MHE. JANET Z. MBENE (K.n.y MHE. SIXTUS R. MAPUNDA) aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko kubwa la kampuni kubwa kuanzisha mashamba ya Kahawa katika maeneo ya Wilaya ya Mbinga na sehemu za Songea Vijijini jambo linalotishia uzalishaji na soko kwa Wakulima wadogowadogo wa Kahawa.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalinda wakulima wadogo wasimezwe na wakulima wakubwa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi ningependa kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Paphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwepo na ongezeko la kuanzishwa kwa mashamba makubwa ya Kahawa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na Wilaya za Mbinga na Songea Vijijini. Hali hii inachangiwa na sera na mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo nchini. Aidha, uwepo na uanzishwaji wa mashamba makubwa nchini hautishii uzalishaji na soko la kahawa kwa Wakulima wadogo wa Kahawa bali una manufaa yafuatayo:-
(i) Uanzishwaji wa uwepo wa mashamba makubwa unawezesha wakulima wadogo walio karibu na mashamba hayo kujifunza teknolojia mbalimbali zinazotumiwa na mashamba hayo katika kuongeza tija na uzalishaji wa kahawa.
(ii) Baadhi ya mashamba makubwa yanaendesha miradi ya kuwasaidia wakulima wa kahawa walio karibu na mashamba hayo (out growers schemes) kwa kuwapa huduma mbalimbali ikiwa ni pamoja na huduma za ugani, ukoboaji na masoko ya Kahawa yao. Kwa mfano, shamba la AVIV lililopo Lipokela Halmashauri ya Wilaya ya Songea limekuwa likitoa huduma za ugani kwa wakulima wanaolizunguka. Aidha, mpaka sasa kiasi cha miche 550,000 imekwishagawanywa kwa wakulima tangu shamba hilo lianzishwe miaka minne iliyopita.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na manufaa hayo, Serikali ilifanya marekebisho ya Kanuni zinazoongoza tasnia ya Kahawa ili kuwalinda wakulima wadogo wanaoingia makubaliano ya uzalishaji wa Kahawa na makampuni binafsi pamoja na mashamba makubwa.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-
Mji wa Mbinga ni miongoni mwa Miji inayokua kwa kasi hapa nchini, hali inayopekekea ongezeko la hitaji kubwa la huduma ya maji safi na salama:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta mradi wa uhakika wa maji safi na salama utakooweza kuwahudumia wananchi wa Mbinga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutatua tatizo la maji kwa muda mrefu kwa mji wa Mbinga, Serikali imeweka mji huo katika mpango wa utekelezaji wa Program ya Maendeleo ya Sekta ya Maji Awamu ya Pili. Lengo ni kusambaza maji safi na salama kwa wakazi wote wa Mji wa Mbinga pamoja na kujenga Kituo cha Kutibu Majitaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zitakazotekelezwa ni pamoja na ulazaji wa bomba kuu, mabomba ya usambazaji, ujenzi wa Kituo cha Kutibu na Kusafisha Maji, jengo la kuhifadhi madawa, ukarabati wa mantanki yaliyopo, ujenzi wa matanki mapya na ujenzi wa Kituo cha Kutibu Majitaka. Mhandisi mshauri amekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na uandaaji wa makabrasha ya zabuni. Utekelezaji wa mradi huu utagharimu Dola za Marekani shilingi milioni 11.86.
Mheheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kutoka kwa wafadhili mbalimbali kwa ajili ya kutekeleza mradi huo. Kwa sasa Serikali imewasilisha andiko la mradi huo, BADEA kwa ajili ya kupata fedha za utekelezaji.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko la Kampuni kubwa kuanzisha mashamba ya kahawa katika maeneo ya Wilaya ya Mbinga na sehemu za Songea Vijijini jambo linalotishia uzalishaji na soko kwa wakulima wadogo wadogo wa kahawa:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalinda wakulima wadogo wasimezwe na wakulima wakubwa?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwepo na ongezeko la kuanzishwa kwa mashamba makubwa ya kahawa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na Wilaya za Mbinga na Songea Vijijini. Hali hii inachangiwa na sera na mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo nchini. Aidha, uwepo wa uanzishwaji wa mashamba makubwa nchini hautishii uzalishaji na soko la kahawa kwa wakulima wadogo wa kahawa bali una manufaa yafuatayo:-
Kwanza, uanzishwaji na uwepo wa mashamba makubwa unawezesha wakulima wadogo walio karibu na mashamba hayo kujifunza teknolojia mbalimbali zinazotumiwa na mashamba hayo katika kuongeza tija na uzalishaji wa kahawa.
Pili, baadhi ya mashamba makubwa yanaendesha miradi ya kuwasaidia wakulima wa kahawa walio karibu na mashamba hayo katika maana ya (outgrowers schemes) kwa kuwapa huduma mbalimbali ikiwa ni pamoja na huduma za ugani, ukoboaji na masoko ya kahawa yao. Kwa mfano, Shamba la Aviv lililopo Lipokela, Halmashauri ya Songea limekuwa likitoa huduma za ugani kwa wakulima wanaolizunguka. Aidha mpaka sasa kiasi cha miche 550,000 imekwisha gawanywa kwa wakulima tangu shamba hilo lianzishwe miaka minne iliyopita.
Mheshimiwa Spika, pamoja na manufaa hayo, Serikali ilifanya marekebisho ya Kanuni zinazoongoza tasnia ya kahawa ili kuwalinda wakulima wadogo wanaoingia makubaliano ya uzalishaji wa Kahawa na makampuni binafsi pamoja na mashamba makubwa.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA (K.n.y. MHE. JOHN J. MNYIKA) aliuliza:-
Askari Polisi wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Kimara wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu kwani kituo ni kidogo na maslahi yao yamekuwa duni:-
(a) Je, ni wapi na lini kituo kipya kitajengwa ili kuboresha huduma na usalama Jimboni Kibamba?
(b) Je, hatua gani zimechukuliwa kuboresha maslahi ya Askari hao ikiwa ni pamoja na kuwaongezea motisha?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA (K.n.y. NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika, Mbunge wa Kibamba, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kipolisi Kimara ilianzishwa kufuatia kuundwa kwa Kanda Maalum ya Polisi Dar es Salaam chini ya Mpango wa Maboresho ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2006 kwa lengo la kuboresha ufanisi na kuongeza huduma za ulinzi na usalama kwa wananchi. Kutokana na uhaba wa rasilimali fedha, huduma za polisi zilianza kutolewa katika jengo la kituo kidogo cha Polisi Mbezi Luis.
Mheshimiwa Naibu Spika, jengo hilo halikidhi hadhi ya kuwa Kituo cha Polisi Wilaya na pia lipo kwenye hifadhi ya barabara kuu ya Morogoro. Serikali itajenga kituo kipya eneo la Luguruni muda wowote kuanzia sasa. Aidha, hali ya vitendea kazi imezidi kuboreshwa ambapo hivi karibuni Wilaya ya Kimara imepatiwa gari lingine lenye namba PT 3696 Toyota Land Cruiser kuimarisha ulinzi wa eneo hilo.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuboresha maslahi ya kuongeza motisha kwa askari wa Jeshi la Polisi, hivi karibuni Serikali imeongeza posho ya chakula, yaani Ration Allowance toka shilingi 180,000 hadi kufikia shilingi 300,000 kwa mwezi, kupandisha viwango vya mishahara sambamba na kuendelea kutoa huduma ya Bima ya Afya.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-
Hospitali ya Wilaya ya Mbinga inatoa huduma kwa Halmashauri Nne yaani Mbinga Mjini, Mbinga Vijijini, Nyasa na baadhi ya Kata za Songea Vijijini, hali inayopelekea Hospitali hiyo kuwa na upungufu wa vitendeakazi, wodi na vyumba vya kulaza wagonjwa pamoja na ukosefu wa Madaktari Bingwa:-
Je, ni lini Serikali itaboresha Hospitali hiyo ili iweze kutoa huduma inayotarajiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MTAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kutatua tatizo la vitendea kazi, Serikali inashirikiana na wadau mbalimbali ili kuboresha huduma za afya. Serikali kupitia wadau ambao ni wattereed imefanikisha upatikanaji wa gari la wagonjwa lenye namba DFP 5795 ambalo linatumika kuhudumia wagonjwa wanaohitaji rufaa. Wadau hao pia wamesaidia upatikanaji wa mashine muhimu za kupima CD4 na maradhi ya kifua kikuu pamoja na kuwezesha ukarabati wa jengo la maabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa wodi ya watoto na ufinyu wa wodi ya wazazi. Aidha, majengo ya wodi ya upasuaji, wodi ya wanaume, wodi ya daraja la kwanza na kliniki ya meno ni chakavu. Katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya watoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya Madaktari (Medical doctors) katika hospitali ni nane, waliopo ni wawili na upungufu ni madaktari sita. Aidha, Madaktari wasaidizi wanaohitajika ni 16, waliopo ni sita na upungufu ni Madaktari 10. Halmashauri imepata kibali cha kuajiri Madaktari wanne katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016. Madaktari watatu waliokuwa masomoni wanatarajiwa kuripoti kazini mwaka huu 2016.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-
Moja kati ya changamoto zinazowakabili wakulima wa kahawa ni kodi na makato mengi:-
Je, ni lini Serikali itazipiga marufuku kodi zote zinazomnyonya mkulima?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto mbalimbali katika uzalishaji wa kahawa nchini ikiwemo kodi na tozo mbalimbali zinazotozwa kwa wakulima na wadau wengine katika tasnia ndogo ya kahawa ambazo zimekuwa na athari katika mapato ya wakulima. Serikali imedhamiria kupunguza na kuondoa kodi na tozo mbalimbali za mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi zisizokuwa na tija ili kupunguza mzigo wa makato kwa wakulima, wafugaji na uvuvi na hivyo kuongeza kipato na kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara katika sekta ya kilimo kwa kupitia upya taratibu, vibali, tozo, kodi, ushuru na ada mbalimbali zinazotozwa ili kupunguza gharama za kufanya biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kutekeleza mkakati wa kupunguza kodi, tozo na ada mbalimbali kwa wakulima, Serikali katika mwaka 2016/2017, imefuta baadhi ya tozo katika mazao ya kilimo, ikiwemo ada ya leseni ya kusindika kahawa ya Dola za Kimarekani 250. Aidha, katika mwaka 2017/2018, Serikali imepanga kuondoa na kupunguza baadhi ya kodi, tozo na ada katika mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi, ikiwemo zao la kahawa ili kuongeza mapato ya wakulima na kuboresha mazingira ya ufanyaji wa biashara katika kilimo, mifugo na uvuvi. Mpango wa muda mrefu wa Serikali ni kuhakikisha kodi, tozo na ada mbalimbali ambazo ni kero kwa wakulima wa kahawa zinafutwa na kubakia na kodi, tozo na ada ambazo zina mahusiano na uendelezaji wa zao husika.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-
Kwa zaidi ya miaka kumi sasa Serikali imejenga jengo la ghorofa moja kwa ajili ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mbinga lakini jengo hilo bado halijakamilika, ujenzi umesimama kwa muda mrefu hali inayosababisha jengo hilo kuharibika na kuanza kupoteza ubora wake. Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukamilisha ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wilaya ya Mbinga, Serikali imetenga shilingi milioni 250 katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018. Fedha hizo zitatumika kukamilika ujenzi wa tanki la maji, uwekaji wa mfumo wa maji safi na maji taka, ujenzi wa uzio, ufungaji wa mfumo wa umeme,vifaa vya kuzuia moto, upigaji rangi na kukamilisha kazi ya nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwasihi kwamba fedha hii itakapotolewa wahakikishe jengo hili linakamilika na kuanza kutumika mara moja.
MHE. MARIAM N. KISANGI (K.n.y. MHE. SIXTUS R. MAPUNDA) aliuliza:-

Tangu mwaka 2016, Serikali iliahidi kuboresha huduma za afya katika Hospitali ya Wilaya ya Mbinga ikiwa ni pamoja na kujenga wodi ya watoto, chumba cha upasuaji na gari la wagonjwa:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya Hospitali ya Halmashauri ya Mji Mbinga ambapo kupitia mapato yake ya ndani Halmashauri ya Mji Mbinga imefanya ukarabati wa jengo la „Grade A‟ kwa gharama ya Shilingi milioni 45 na kununua jokofu la kuhifadhia maiti lenye thamani ya Shilingi milioni 29.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali imetoa kiasi cha Shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kalembo ili kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji Mbinga, ahsante.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Vijiji vya Mpepai na Lipilipili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sixtus Raphael Mapunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mradi wa kusambaza umeme vijijini katika vijiji vyote vya Tanzania Bara. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2021. Mradi wa REA III unaoendelea utapeleka umeme katika vijiji 50 vya Wilaya ya Mbinga kupitia Mkandarasi Namis Corporate Ltd anayetekeleza kazi hiyo katika Mkoa wa Ruvuma.

Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Mpepai na Lipilipili pamoja na vijiji vingine vilivyobaki katika Wilaya ya Mbinga vitapatiwa umeme kupitia Mradi unaoendelea. Kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vya Mpepai na Lipilipili inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 18, ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 22, ufungaji wa transfoma nane za KVA 50, 100 na 200, pamoja na kuwaunganishia huduma ya umeme wateja wa awali 313. Gharama ya mradi ni shilingi milioni 977.