Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Anthony Peter Mavunde (1 total)

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE Aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuliendeleza zao la zabibu Mkoani Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anthony Peter Mavunde, Mbunge wa Dodoma Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa zabibu kwa sasa ni wastani wa tani 16,000 kwa mwaka ukilinganisha na uwezo uliopo wa kuzalisha zabibu wastani tani 150,000 kwa mwaka. Mahitaji ya mchuzi wa zabibu kwa mwaka ni wastani wa lita milino 15 ambapo uzalishaji wa ndani wa nchi kwa mwaka tunazalisha wastani wa lita milioni 5 na jumla ya lita milioni 10 zinaagizwa kutoka nje zenye thamani ya dola milioni 6. Sasa Serikali imeliingiza zao la zabibu kuwa mingoni mwa mazao ya kimkakati ambayo yamepewa kipaumbele katika kuendelezwa n Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza zao la zabibu Serikali imeweka mikakati mbalimbali ikiwemo kuhakikisha upatikananaji wa miche bora kupitia TARI na halmashauri za wilaya husika, kuimarisha huduma za ughani katika zao la zabibu, kuongeza upatikanaji wa soko kutoka wastani wa asilimia 65 hadi 85, kuongeza tija ya uzalishaji wa tani 6.25 kwa hekta hadi kufika tani 30 ifikapo mwaka 2025. Vilevile kuweka mazingira bora ya uwekezaji katika tasnia ya zabibu, kufufua na kuanzisha mashamba makubwa ya zabibu na kutenga na kulinda ardhi kwa ajili ya kilimo cha zabibu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuijengea uwezo TARI kuendelea na utafiti na kuzalisha miche kwa kuongeza bajeti ya utafiti wa mazao ya kilimo ikiwemo zao la zabibu kutoka shilingi bilioni 7.3 mwaka 2021 hadi kufika bilioni 11.63 mwaka 2021/2022.

Aidha, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuwanunulia vitendea kazi Maafisa Ugani ambao hawana vyombo vya usafiri katika Mkoa wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, Serikali pia imeweka mkakati wa kufufua mashamba makubwa ya zabibu ambayo uzalishaji wake unasuasua. Katika kutekeleza adhima hiyo Serikali imefufua shamba la Chinangali II lenye ukubwa ekari 602 lilipo Wilaya ya Chamwino kwa kukarabati bwawa la maji na visima vilivyopo shambani.