Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Dr. Joseph Kizito Mhagama (1 total)

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu Swali. Mheshimiwa Waziri Mkuu moja katika mikakati ya Serikali, ili kuinua sekta ya kilimo ni kuhakikisha kwamba, wakulima wadogo walioko vijijini wanapata pembejeo katika ubora na katika viwango vinavyokusudiwa. Na hilo litafanikiwa tu pale ambapo mfumo wa ufikishaji pembejeo kwa Wananchi ni mfumo endelevu ambao utahusisha kuwepo na maduka madogo-madogo vijijini ya pembejeo ambayo yataweza kuuza mbolea, mbegu bora pamoja na viuatilifu.

Mheshimiwa Spika, lakini imebainika kwamba, jitihada za wadau pamoja na Serikali za kuhakikisha kwamba, kunakuwa na maduka madogo-madogo ya pembejeo vijijini zinakwamishwa na gharama kubwa ya kufuzu kuwa na maduka hayo, ikiwemo gharama kubwa kwenye TOSKI zaidi ya laki moja na eneo la TPRA ambalo laki tatu na gharama nyingine ambazo zinamfanya mdau anayetaka kuwekeza kwenye sekta hiyo, lazima atumie zaidi ya 600,000 kabla hajanunua malighafi kwa ajili ya duka lake.

Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba, inapunguza au kuondoa gharama hizo, ili kufikia malengo tuliyojiwekea ya kuhakikisha mkulima mdogo ananufaika kwa kupata pembejeo bora na salama kwa ajili ya uzalishaji?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhagama, Mbunge wa Madaba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali limekuwa na maelezo mengi, lakini msingi wake anataka kujua Serikali ina mpango gani wa kutoa, kupunguza tozo za maduka yanayouza pembejeo, ili kumuwezesha mkulima kupata pembejeo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali imepokea ushauri na vilevile malalamiko kadhaa kutoka kwa wafanyabiashara mbalimbali wakiwemo hao wanaofungua maduka ya pembejeo juu ya tozo mbalimbali katika uendeshaji wa shughuli nzima za biashara. Nataka nikuhakikishie kazi kubwa inayofanywa na Serikali sasa ni kufanya mapitio ya tozo zote kuanzia kwa wakulima kwenye mazao yao, kwa wafanyabiashara wenyewe wanapofanya biashara, ili kutengeneza mazingira mazuri ya kufanya biashara nchini, ikiwemo maduka hayo yanayosambaza pembejeo, ili kufikisha pembejeo kwa urahisi kwa mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mawaziri wenye dhamana ambao wana tozo mbalimbali kwenye Wizara zao zinazokwamisha kufanya biashara katika mazingira rahisi wameshakutana. Na hata juzi nilikuwa na Mawaziri hao kupata taarifa zao kwa pamoja kuona maeneo yote waliyoyapitia na tozo zote ambazo zinataka kupitiwa upya na kazi hiyo inayoendelea sasa ikishakamilika sasa watakutana pia na Kamati ya Bajeti ya Bunge, watakutana pia na Wizara ya Fedha, ili kuona namna nzuri ya kuondoa tozo hizo, lakini badae itaenda kwenye mamlaka inayotoa ridhaa ya kuondoa kodi ikiwemo na hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jitihada za Serikali katika hiyo zimeshaanza na tutakapofikia hatua nzuri tutakagua pia na maeneo unayotaja ya maduka yanayouza pembejeo, ili kuwawezesha wafanyabiashara wa maduka hayo kupata pembejeo na kuzipeleka mpaka ngazi ya kijiji, ili wakulima waweze kupata pembejeo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkakati wa Serikali unaendelea na niwape matumaini wafanyabiashara wote nchini kwamba, Serikali imewasikia vilio vyao na sasa tunafanya mapitio ya tozo hizo, tutakapofikia hatua nzuri tutawajulisha na tutawashirikisha katika kujua ni aina gani ya tozo ambayo tunataka tuiondoe na au kuibadilisha kwa namna moja au nyingine, ili muendelee kufanya biashara zenu katika mazingira rahisi.