Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Fatma Hassan Toufiq (75 total)

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kwamba hadi sasa hivi katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma pesa ambayo imeidhinishwa mwaka 2014/2015 haijatolewa na pia ya 2015/2016 haijatolewa:-
(i) Je, ni lini pesa hizi zitatolewa ili kukamilisha ujenzi huo?
(ii)Je, Serikali haioni kwamba inaingia gharama za ziada inapochelewesha miradi na kuathiri mipango ya wale wakandarasi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lini Serikali itakuwa tayari kutoa pesa hizo, jibu kwa ufupi ni kwamba pesa hizo kwa kuwa zipo kwenye bajeti, zitatolewa pindi Serikali itakapopata pesa za kutosha na ambazo zitakuwa tayari kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusu variation ambayo inatokana na kuchelewa kwa miradi, kwa bahati mbaya sana kuna gharama nyingine haziepukiki kutokana na uwezo mdogo wa kiuchumi wa nchi yetu. Nia thabiti ipo na utekelezaji utafanyika tu pale ambapo tutaweza kuwa na fedha hizo. Kwa bahati mbaya sana kama tutakuwa tumeshaingia gharama hatutakuwa na namna ya kuzikwepa kwa kuwa ndiyo hali halisi ya uchumi wetu.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa Serikali haijaanza kupokea maoni, je, imepangaje kushirikisha wanawake wengi zaidi katika kutoa maoni yao?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Wizara itaanza lini maandalizi ya kuchukua maoni hayo? Ahsante!
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara pamoja na Tume ya Kurekebisha Sheria imepanga kulifanya zoezi hili kama tulivyoelekezwa mwanzoni kwa kina na kwa kuwafikia wananchi wengi kadri iwezekanavyo na ndiyo sababu ya Baraza la Mawaziri kusema tusileta mabadiliko hapa bila kutumia utaratibu wa white paper ambao una lengo la kuwafikia wananchi wengi iwezekanavyo.
Kwa hiyo, tutahakikisha wanawake wengi iwezekanavyo tunawafikia na natoa wito kwa wananchi wote na wanawake wote Tanzania pale watakaposikia mchakato umeanza naomba wajitokeza kutoa maoni kuhusu sheria hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusu maandalizi yanaanza lini, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Fatma Toufiq kwamba maandalizi yalishaanza na sasa hivi tunapitia nyaraka zote za mwanzo ziendane na hali halisi ya leo.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa Mkoa wa Dodoma una mifugo mingi na kunahitajika kiwanda cha kuchakata mazao ya mifugo; Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kiwanda hicho katika Mkoa wa Dodoma?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Toufiq. Mpango wa Serikali ni kujenga viwanda vya kuchakata nyama, huu ni mkakati pamoja na faida ya zao hili la nyama, tunalenga kutumia njia hii kuwashawishi wafugaji waweze kutoa mifugo yao kwenye sehemu za hifadhi. Kwa hiyo Sekta binafsi inahamasishwa na tuna machinjio hapa, tunategemea kutengeneza Kongwa, Ruvu, na tunaimani kwamba kwa kuwa na Kongwa na machinjio ya Dodoma kiwanda kitaweza kutangamka. Lakini nichukue fursa hii kukuomba Mheshimiwa Mbunge, ukimuona Mwekezaji yeyote mwambie aje awekeze Dodoma, mimi ninazo ekari 200, kama anataka kuwekeza aje tushirikiane nitampa eneo, ajenge sehemu ya kuchakatia, machinjio tunayo ni sehemu ya kuchakatika nyama tu.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Meshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, je, Mswada huu wa Sheria ya Makao Makuu utaletwa Bungeni mwaka huu?
Swali la pili, je, bajeti kwa ajili ya mchakato huu imetengwa katika kipindi hiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (WATU WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kama Muswada huu utaletwa mwaka huu au la kwa kweli itategemea hasa na majibu yatakayotokana na kikao cha wataalam. Kwa hiyo, kama maoni yao hayatokuwa na marekebisho mengi ni wazi kwamba muswada huu utaletwa mapema. Lakini kama maoni yao yatasababisha marekebisho makubwa katika muswada huu, basi muda unaweza ukahitajika zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili kuhusu suala la bajeti ni wazi kwamba bajeti haiwezi ikawa imepangwa kipindi hiki, kwa sababu sheria hiyo bado haijapita, na kwa vyovyote vile sheria itakapopitishwa Bungeni, itaweka wazi muda wa kuanza utekelezaji wake na kwa wakati huo ndio bajeti itapangwa.
MHE. FATMA HASSAN TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imeshakamilisha hatua za kuwasilisha muswada huu, je, ni lini muswada huu utawasilishwa Bungeni?
Swali la pili, je, Serikali ina mpango wowote wa kuandaa mtaala wa Wasaidizi wa Kisheria ili wote waweze kupata mafunzo kulingana na mtaala huo? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Fatma Toufiq kwa maswali yanayogusa wananchi wa kawaida na hili suala kwa kweli hata sisi kama Wizara tunaona ni muhimu na ndiyo maana tumelifuatilia kwa karibu na Serikali imeridhia tuweze kuja na muswada huo ambao utajadiliwa na Bunge.
Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya taratibu kukamilika, muswada huu hautakuja moja kwa moja Bungeni hapa lakini utapitia katika Kamati, pia tutakuwa na mjadala wa muda mrefu kabla ya kuja na text ambayo Waheshimiwa Wabunge mtakuja kuijadili.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maandalizi ya kutosha tumeyafanya, kwa mfano, sasa hivi tuna mitaala kabisa iliyowekwa kwa ajili ya kuwafundisha hawa Wasaidizi wa Sheria. Ni kazi kubwa imefanywa na Chama cha Wanasheria Tanganyika na ninaomba nimhakikishie tu kwamba tumejiandaa vizuri sana kubeba hili jukumu.
Tunasema hivyo kwa sababu Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaongelea kuhusu usawa mbele ya sheria. Tunaamini Muswada huu unatupeleka Watanzania karibu zaidi katika kukidhi mahitaji ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ili uwepo usawa wa kutosha kabisa mbele ya sheria.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali moja la nyongeza.
Je, Serikali imeandaa utaratibu wowote wa kuwakagua watoto ambao wapo chini ya umri wa miaka mitano katika kliniki au wasiohudhuria kliniki ili kuweza kupata takwimu sahihi za watoto ambao wamekeketwa chini ya miaka mitano ili kufahamu ukubwa wa tatizo ukoje? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ni kwamba katika mfumo wa kutoa huduma za afya nchini watoto wote chini ya umri wa miaka mitano wanapaswa kuhudhuria kliniki ya RCH ili wapate chanjo mbalimbali lakini pia wazazi wao waweze kufikiwa na elimu mbali mbali ambazo zinatolewa kila siku kabla ya kuanza kwa kliniki hizo.
Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na utaratibu huo watoto wote wachanga sasa hivi kuna mpango maalum chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wa kuwaelimisha wauguzi wote nchini kufanya ukaguzi maalum wa watoto hususani wa kike kuhusiana na mambo ya ukeketaji ili tuweze kuwabaini wazazi ambao wamewapeleka watoto wao wachanga kufanyiwa ukeketaji.
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo huduma hiyo sasa ipo na inaendelea kutolewa nchini. Nitoe onyo kwa wazazi wote ambao wanaendelea na vitendo hivi, kwamba wakikamatwa hatua kali zitachukuliwa dhidi yao kwa sababu kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi utaratibu umehama badala ya kuwakeketa mabinti wakubwa, sasa hivi wazazi wamegundua kwamba wawakekete watoto wachanga. Jambo hili halikubaliki na tutachukua hatua kali, na ndiyo maana tumeweka sasa mkakati wa kutoa elimu kwa wauguzi wafanye ukaguzi maalum kwa watoto wa kike kama wamekeketwa ama la, kwa hiyo utaratibu upo.
MHE FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa
Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imeanzisha Mfuko wa Udhamini wa UKIMWI na imetenga kiasi cha shilingi bilioni 5.6 kwa ajili ya mfuko huo, je, Serikali haioni umuhimu wa kutumia sehemu ya pesa za mfuko huo kwa kutoa ruzuku kwa kiwanda hicho?
Swali la pili, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kuwa uzalishaji unaanza mapema zaidi ili kupunguza gharama za kuagiza dawa za ARV kutoka nje? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye Mfuko huu wa UKIMWI kwa mujibu wa sheria uko chini ya Ofisi hiyo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba nijibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Waziri mwenzangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu ambaye ni mdau mkubwa tunayefanya naye kazi kwa pamoja kushughulikia masuala haya ya tatizo la UKIMWI nchini kwa majibu mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfuko huu ambao unashughulikia matatizo ya UKIMWI (ATF) umeanzishwa kwa mujibu wa sheria na sheria imeweka mamlaka kwa bodi inayosimamia mfuko huo kutoa miongozo na kuangalia ni kwa namna gani fedha zitakazopatikana kwenye mfuko
zitatumika kwa ajili ya shughuli mbalimbali zinazoendana na tatizo la UKIMWI katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bodi imeshagawa utaratibu wa matumizi ya fedha hizo kwa asilimia 60 kutumika kwenye matibabu, dawa na vitendea kazi na asilimia nyingine 25 na 15 kwa kazi nyingine.
Kwa hiyo, kwa utaratibu ama ushauri ambao ameutoa Mheshimiwa Mbunge, tutarudi kuwasiliana na bodi kuona kama katika zile asilimia 60 zinaweza pia zikatumika katika kusaidia utengenezaji wa dawa kwenye nchi yetu ya Tanzania kama mfuko utakuwa umeshajitosheleza kwa kiasi kikubwa na kiasi cha kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kupokea ushauri wa kuboresha matumizi ya fedha ya mfuko huo kadiri inavyoonekana inafaa.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru
Mheshimiwa Jenista kwa kujibu sehemu ya kwanza ya swali hili, kati ya maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fatma Toufiq.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili, Serikali ina mikakati gani ya kuhakikisha tunawekeza katika uzalishaji
wa dawa za ARV nchini Tanzania? Nataka kumthibitishia Mheshimiwa Mbunge kwamba hadi sasa tuna viwanda
vitano, wawekezaji watano ambao wameonesha nia ya kutaka kuwekeza katika uzalishaji wa viwanda vya dawa
nchini na wiki iliyopita tulikuwa pale Bagamoyo, Zinga Phamaceutical Company na moja ya dawa ambayo
watazalisha ni pamoja na dawa za kupunguza makali ya UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka tu kumthibitishia tunafanya kazi pia pamoja na Mheshimiwa
Charles Mwijage kuhakikisha kwamba tunazalisha dawa zetu zote ndani ya nchi badala ya kununua dawa nje ya nchi kama tunavyofanya sasa hivi.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa, Serikali imeona umuhimu wa kufufua na kurejesha majengo ya maendeleo ya jamii. Je, Serikali ina mkakati gani wa kupata wataalam wa kutosha ili kuhudumu katika majengo hayo?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, hali ya maisha imebadilika sana na wananchi wengi wana msongo wa mawazo na matatizo mbalimbali, mfano, masuala ya ukatili, hivyo wanahitaji wataalam wa unasihi na nasaha. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka muda maalum ili kuharakisha Halmashauri zote nchini zifufue majengo hayo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Ni kweli tumekuwa na changamoto kubwa sana ya watumishi katika Sekta nzima ya Maendeleo ya Jamii na hivi sasa tuna upungufu wa asilimia takribani 61. Hata hivyo, Serikali imeendelea kuchukua jitihada mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuongeza udahili katika mafunzo ya watumishi katika sekta hii, mpaka sasa hivi tumeongeza udahili kwa kiasi kikubwa sana. Lengo ni kuhakikisha kwamba sasa huu upungufu tulionao tunaweza tukapata watumishi wa kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali lake la pili kwamba, kutokana na kuonekana kuna wananchi wengi sasa hivi wamekuwa na msongo wa mawazo, tunapokea ushauri huu nasi katika sekta ya afya tutaangalia njia nzuri zaidi ya kuweza kulifanyia kazi jambo hilo.(Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii kuweza kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kumekuwa na tatizo la uwekaji kiholela wa matuta kwenye baadhi ya barabara za mitaani na hivyo kusababisha usumbufu mkubwa kwa watumiaji wa vyombo vya moto na ikizingatiwa kwamba wananchi hawa hawana utalaam wowote. Je, Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na kadhia hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokuwa namueleza Mheshimiwa Joseph Mhagama, ninatoa wito kwa Watanzania, barabara hizi zinajengwa kwa gharama kubwa sana ya pesa za Watanzania. Tunapoweka matuta bila vyombo vinavyohusika hasa TANROADS kufahamu tunaharibu barabara zetu ambazo tumezijenga kwa gharama kubwa sana. Kitu ambacho Serikali tunakifanya, tunapanga mkakati wa kuwasiliana na Wizara ya mambo ya ndani kitengo cha usalama barabarani kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi namna ya matumizi bora ya barabara bila kuleta ajali kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaomba sana Watanzania wasijichukulie maamuzi ya kuweka matuta barabarani hata kwa kugongwa kwa mbuzi tu isipokuwa wawasiliane na taasisi zinazohusika tusaidie kama kuna umuhimu wa kuweka matuta tutaweka, lakini kwa utaratibu ambao unaeleweka.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa tatizo lililopo katika jimbo la Kibiti linafanana na baadhi ya maeneo katika mji wa Dodoma, kwamba baadhi ya mitaa mfano Nkuhungu, Ilazo, Makole barabara zake za mitaa zipo katika hali duni sana. Je, Serikali itarekebisha lini barabara hizi ukizingatia kwamba sasa hivi Dodoma ni Makao Makuu? Ahsante.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu wazi hoja anayozungumza Mheshimiwa Fatma Toufiq kwamba ni kweli ni hoja halisia. Hii ni kwa sababu mji wetu wa Dodoma sasa hivi kwa maamuzi sahihi yaliyofanywa Serikali ni Makao Makuu yetu. Hata hivyo kupitia miradi yetu ambayo tunaendelea nayo hapa Dodoma, sawasawa na miradi ambayo tunaendelea nayo katika miji saba katika ile Strategic City Project; kazi hii inaendelea awamu kwa awamu. Wabunge nadhani mnakuwa ni mashahidi. Wabunge waliofika mwaka 2010 hapa Dodoma wakifanya ulinganifu na hali ilivyo hivi sasa ni tofauti sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo tutaendelea kujenga miundombinu hii. Sasa hivi kuna ring road karibuni zitakuwa tatu. Kuna hii ambayo hata ukifika kule inakatisha, vilevile tuna barabara zetu za mitaa na wataalam wetu wanaendelea na kazi hiyo. Lengo letu ni kwamba tukifika mwaka 2020 Jiji la Dodoma litakuwa ni tofauti sana kwa sababu mpango wetu huo ambao unaenda mpaka mwaka 2020 utahakikisha mji wa Dodoma wote mitaa yake yote itakuwa na kiwango cha barabara za lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo si lami peke yake isipokuwa tutapeleka na mataa pamoja na mifereji yote ya kuondoa maji kuhakikisha jiji hili linakuwa jiji la mfano ambao ndio mpango hasa wa Serikali yetu ilivyoamua.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa kuweza kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa hizi ajali za barabarani zinatokana na uzembe wa baadhi ya madereva na baadhi ya madereva kutumia simu wakati wakiwa wanatumia vyombo ya moto. Je, Serikali ina mkakati gani wa kurekebisha Sheria ya Usalama Barabarani ili kuwachukulia hatua kali zaidi hawa madereva ambao wamekuwa wakitumia simu wakati wakitumia vyombo vya moto? Ahsante.
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kweli kuna kiwango kikubwa cha ajali zinatokea kutokana na uzembe. Ukiangalia hata kwenye kumbukumbu zaidi takribani ya matukio zaidi ya 1,500 yanatokana na uzembe.
Mheshimiwa Naibu Spika, kile alichokisema cha kurekebisha sheria na kuchukua hatua tunaendelea na utaratibu huo na tunasema tunakokwenda tutaanza hata kutumia taratibu ambazo nchi zingine wanatumia kwa ku- count down dereva ambaye anapatikana sana na makosa aweze kukosa sifa za kuendelea kumiliki leseni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunalifanyia kazi wazo lake na nimpongeze sana kwa kuguswa na jambo hili kwa sababu limekuwa likisababisha hasara sana kwa familia na kwa Taifa. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante. nashukuru sana kwa majibu ambayo yametolewa na Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa mwekezaji aliyechukuwa DOWICO alizembea na kufunga kiwanda hicho, hivyo kusababisha uzalishaji mvinyo bora wa Dodoma kutokupatikana katika soko. Je, Serikali haioni umuhimu wa kumpatia mwekezaji mwingine tofauti na huyu aliyepo ili aweze kukifufua kiwanda hicho?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali imekuwa katika mpango wa kuwezesha uanzishwaji wa Kiwanda cha Kusindika mazao ya Zabibu katika Wilaya ya Chamwino kwa kushirikiana na mfuko wa GEPF. Je, ni hatua gani za haraka zilizochukuliwa na Serikali ili kuharakisha ujenzi wa kiwanda hiki ili wakulima wa zao la zabibu waweze kupata soko? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU - K.n.y WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI): Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la kwanza la kumtafuta mwekezaji mwingine, ndani ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Viwanda TIRDO na kwa kushirikiana pia na Ofisi ya Msajili wa Hazina tumeanzisha kitu kinaitwa Technical Audit na lengo lake kubwa ni kwenda kuvifuatilia viwanda hivi ambavyo vilibinafsishwa na havifanyi kazi na kuvifuatilia kuona namna gani vitaanza kufanya kazi kwa kupitia utaratibu huo wa utafiti ambao unafanyika.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwondoe hofu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tunawasiliana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na kama nilivyosema katika majibu yangu ya msingi kwamba tayari ukarabati umeanza, kwa hiyo tutafanya hiyo technical audit ya kufuatilia kuona wanaanza lini kazi hii na baadaye tutatoa taarifa namna ya utekelezaji wake.
Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba jambo hili ni kubwa sana kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma, hasa ukiangalia kwamba zabibu ndio zao pekee ambalo linategemewa sana hapa Dodoma na Dodoma ndio sehemu pekee duniani ambako kuna uwezo wa kuvuna zabibu hii mara mbili. Israel wamejaribu, Afrika Kusini wamejaribu imeshindikana, kwa hiyo tunafahamu umuhimu wa zao hili kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma.
Mheshimiwa Spika, nimwondoa hofu Mheshimiwa Mbunge tu kwamba, hii pia ni Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwavutia wawekezaji wengi kujenga viwanda vikubwa hasa ukizingatia kwamba mpaka Machi, 2017 tayari tumeweza kuvutia viwanda vikubwa 393 ambavyo vimesajiliwa na tayari vimeshaweka kiasi cha shilingi trillion tano. Kwa hiyo nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba, hata hili nalo litafanyika
Mheshimiwa Spika, la pili ameuliza kuhusu Kiwanda cha Mvinyo pale Chamwino. Nafahamu wakulima wa Dodoma wanategemea sana viwanda hivi vikubwa kwa ajili ya soko la zabibu, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge katika utaratibu wa uwekezaji katika viwanda, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, iliamua kuingia moja kwa moja katika uwekezaji huu. Pale Chamwino Mfuko wa GEPF, WCEF pamoja na TIB kwa pamoja watafanya uwekezaji wa kiwanda cha mvinyo.
Mheshimiwa Spika, ninavyozungumza hivi sasa tayari Bodi za Mifuko hii zimekwisha-approve kiasi cha shilingi bilioni 26 kwa ajili ya kwenda kuanza ujenzi wa kiwanda hiki. Niwaondoe hofu wananchi wa Mkoa wa Dodoma, watapata fursa ya masoko ya zabibu na ukiongozwa na wewe Mheshimiwa Spika, ambaye ni mkulima pia. (Makofi/Kicheko)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa baadhi ya wazazi na walezi wamekuwa wakiwaficha watoto ambao wamekuwa na ulemavu na hivyo kukosa haki za msingi kama afya na elimu. Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu wazazi na walezi hawa ambao wanawakosesha hawa watoto? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. STELLA I. ALEX): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua na imekuwa ikitoa elimu mara kwa mara kuhusiana na umuhimu wa kwamba kila mtoto mwenye ulemavu anawajibika ama ana fursa sawa na watoto wengine ambao hawana ulemavu. Kwa kuliona hilo hivi ninavyozungumza tayari kuna zoezi linaendelea la kuwatambua watoto wenye ulemavu kila mahali nchini ili kuona sasa ni jinsi ya kuhakikisha kwamba hawafichwi tena ndani na wanapatiwa huduma kama watoto wengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili linafanyika. Hata hivyo niendelee kutoa rai kwa wazazi wote nchini pamoja na walezi kuhakikisha kwamba watoto wenye ulemavu wanawapatia fursa sawa na watoto ambao hawana ulemavu. Mtu mwenye ulemavu ni sawa na mtu mwingine ambaye hana ulemavu, akiwezeshwa anakuwa anaweza. Kwa hiyo, nitoe rai sana na niwaombe wazazi pamoja na walezi kulizingatia hilo kuona kwamba watu wenye ulemavu wako sawa pamoja na watu ambao hawana ulemavu.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa ukosefu wa mabweni ni tatizo la nchi nzima na hasa katika shule za sekondari za kata, hivyo kufanya baadhi ya wanafunzi kupanga katika nyumba za watu binafsi; je, Serikali haioni umefikia wakati kuhamasisha wadau mbalimbali wa elimu kujenga hostel karibu na shule ili kuepuka kadhia hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA): Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalitambua sana tatizo la mabweni katika shule za sekondari za kata. Lengo la kujenga shule za sekondari za kata ilikuwa ni kuwawezesha watoto ambao wako ndani ya kata waweze kusoma, lakini tatizo ni kwamba kuna baadhi ya vijiji kweli viko mbali sana na Makao Makuu ya Kata au mbali sana na eneo ambalo ipo shule. Kwa hiyo, kuna tatizo kwamba wanafunzi wengi wamekuwa wakipanga nyumba kwa sababu hawawezi kutembea kilometa labda 15,20 kutoka nyumbani kwao kwenda katika shule kusoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo tatizo tunalielewa na ninaungana naye na tutaendelea kuhimiza wadau wajenge mabweni na hostel karibu na shule hizi ili kusudi ziweze kutoa huduma nzuri kwa watoto na hasa watoto wa kike waweze kuepuka matatizo mengine ambayo yanawapata kupanga katika nyumba za watu.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa suala la ubakaji na ulawiti linazidi kuongezeka; je Serikali haioni imefika wakati wa kuwa na hotline maalum ya kutoa taarifa za ukatili kwa wale ambao wanapata tatizo hilo?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali imeweka mpango mzuri wa kuwa na dawati la jinsia. Kwa nini Serikali isiweke utaratibu wataalam hawa wakaenda kutoa elimu katika shule zetu mbalimbali hapa nchini? Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi maswali yake yote mawili ni kutoa ushauri na mapendekezo, nimhakikishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mapendekezo ambayo anayotoa, nitayafikisha Serikalini tuone namna ya kuyafanyia kazi. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa tatizo la wahamiaji haramu kutoka Ethiopia linaongezeka, je, Serikali haioni imefikia wakati wa kulizungumza suala hili kidiplomasia kati ya Tanzania na Ethiopia ili kuweka utaratibu maalum kuepuka kuwaweka magerezani ambapo huligharimu Taifa? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu sahihi aliyoyatoa tangu mwanzo na niwapongeze Waheshimiwa Wabunge kwa kulileta swali hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ijumaa na Jumamosi tulikuwa na vikao vya Jumuiya ya Afrika Mashariki vinavyoshughulikia masuala ya kiusalama ya kisekta na kwenye maazimio tuliyoyapitisha ni pamoja jambo hili kuwa jambo la mipaka yote ya Jumuiya ya Afrika Mashariki tofauti na ilivyo sasa ambako nchi zingine zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwepo Kenya wanapopitia zaidi kwao wao hili jambo halikuwa kama tatizo walikuwa wanapita tu kama mtembeaji mwingine yeyote aliyeko ndani ya nchi husika. Kwa hiyo, kwa sasa tumesema hili ni jambo ambalo tutalioanisha na mambo mengine ambayo yanazuiwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ili hawa watu waweze kuanza kuzuiwa kwenye mipaka ya Kenya na Sudan Kusini tofauti na ilivyo sasa ambapo huwa wanapata kipingamizi wanapofika Tanzania na nchi zingine zote wanakuwa wameshapita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tunalipokea na hilo jambo ambalo amelisemea la kuongea nanchi husika ambao wahamiaji hawa wanatoka ambapo ni Ethiopia, Eritrea pamoja na Somalia. Hiyo tutaifanya kwa kuanzia na Balozi zao zilizopo hapa ili jambo hilo liweze kuongewa pia katika nchi zao.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza mswali ya nyongeza, nina maswali mawili ya nyongeza namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa Wizara haidhibiti kope bandia na kucha bandia lakini bado zina madhara makubwa sana kwa watumiaji hasa wanawake.
Je, Serikali haioni umefikia wakati kupitia Wizara ya Afya na TFDA kufanya utafiti ili kubaini ukubwa wa tatizo?(Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amekiri kuwa wagonjwa takribani 700 hupelekwa Muhimbili kutokana na athari za kujibadili rangi.
Je, Serikali haioni umefikia wakati kuwa na mpango kabambe wa kuihabarisha jamii na hasa wanawake kubaki na rangi zao za asili na kuepuka kutumia vipodozi vyenye madhara na hasa wanaume wawe ndiyo waelimishaji? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, tunapokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge wa kufanya tafiti na kubaini madhara ya kucha na kope bandia na baada ya hapo sasa tutaanza kuwa na mfumo wa kuwa na takwimu mbalimbali kuhusiana na madhara haya.
Mheshimiwa Spika, swali la pili ameuliza je, Serikali hatuoni umuhimu wa kuhabarisha jamii kuhusiana na vipodozi ambavyo vinabadilisha rangi ya mwili. Naomba nitumie fursa hii kutoa elimu kidogo kwa Bunge lako tukufu.
Mheshimiwa Spika, Mwenyezi Mungu alituumba na hizi ngozi zetu hizi kwa makusudi yake mahsusi. Kwanza ngozi hizi ni moja ya kinga ya mionzi ya ultraviolets ambayo ngozi inatukinga dhidi yake, lakini pili, ngozi hii ni sehemu ya kinga za mwili ama kizuizi cha kinga ya mwili pale wadudu ama bakteria ama vijidudu vya aina yoyote vinapotaka kuingia katika miili yetu vinazuiliwa na ngozi zetu. Tunapokuwa tunajichubua ngozi zetu tunaziondoa kinga hizi na tunaondoa kinga hii dhidi ya miale hi ya ultraviolet, lakini tunaondoa kinga hii dhidi ya vimelea vya wadudu hatari.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mtu ambaye anafanya kujichubua ngozi anaingia katika madhara ya magonjwa ya ngozi, madhara ya kupata saratani ambayo inatokana na vimelea vilevile miale ya jua. Kwa hiyo, mimi naomba kutoa rai tu kwa Watanzania wote ambao wanatusikiliza na Waheshimiwa Wabunge ngozi zetu za asili ni urembo uliotosha, kama Wabunge tulizingatie hilo na wanaume tushiriki, rangi ya asili... naishia hapo (Makofi/Kicheko)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa baadhi ya shule za msingi zina vituo vya ufundi stadi, mfano, katika Wilaya ya Chamwino, vituo hivyo viko katika Shule ya Msingi Mvumi Mission na Shule ya Msingi Chamwino lakini hakuna vifaa wala walimu wa kutosha. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuvifufua vituo hivyo siyo kwa Wilaya ya Chamwino tu lakini katika shule zote za msingi ambazo ziko Tanzania hii? Ahsante.
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLIJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la dada yangu Mheshimiwa Fatma Toufiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru kwa swali lake zuri kwa sababu ni kweli zile shule zipo lakini kwa kweli hali yake haijakaa vizuri, niliona nilipozitembelea. Kwa hiyo, tayari Serikali imeliona na kwa kupitia Mradi wa Kukuza Ujuzi hapa Nchini (ESPJ) ambao Wizara yangu inautekeleza kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, tutafanya tathmini ya shule hizo na kwa awamu tutaanza kuzifanyia maboresho kwa kuzipelekea vifaa.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa tatizo lililopo katika Mkoa wa Mtwara linafanana na kukatika kwa umeme katika eneo la Kigogo Mkoani Dar es Salaam tena bila taarifa; je, Serikali ina mkakati gani wa kukabiliana na kadhia hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Toufiq amekuwa akifuatilia mara kwa mara suala hili la kukatika kwa umeme kwa maeneo ya Kigogo. Kupitia mpango wa Serikali na Shirika lake la TANESCO, tunajenga sub-station maeneo ya Mburahati ambapo sub-station hiyo itasaidia kumaliza kabisa tatizo la kukatika kwa umeme maeneo ya Kigogo. Nakushukuru.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa nami kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Chuo cha Ufundi VETA, Dodoma kilijengwa muda mrefu na kilikidhi kwa wakati ule na sasa hivi kuna ongezeko kubwa sana la vijana na miundombinu bado ni ile ile; je, Serikali haioni kwamba umefikia wakati wa kuongeza majengo na miundombinu ili kiendane na hadhi ya Jiji? Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali ina mpango wa kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika vyuo vyote nchini, na sio Vyuo vya Ufundi tu. Kwa hiyo, tutaendelea kuangalia vyuo vile ambavyo vinahitaji matengenezo na ukarabati pamoja na kuongezewa Majengo, ili tuweze kufanya hivyo kadiri bajeti itakavyoturuhusu.
Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie tu kwamba, hata Chuo cha Dodoma nacho ni moja kati ya vyuo tulivyonavyo na kwa vyovyote vile kulingana na upatikanaji wa fedha tutaangalia uwezekano wa kukipanua.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa soka la wanawake limekuwa likifanya vizuri sana hapa nchini na kimataifa, lakini soka hili halina wadhamini wa kulidhamini. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuhamasisha wadau mbalimbali ili waweze kulidhamini soka hili la wanawake nchini? (Makofi)
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, soka la wanawake pamoja na kwamba limechelewa sana kupewa uzito stahili katika nchi yetu, tayari lina wadhamini. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Toufiq kwamba kila mwaka tunazidi kuongeza juhudi za kuwapata wadhamini. Moja ya nyenzo kuu ya kuwapata wadhamini wengi zaidi ni kuhakikisha kwamba tunaomba au tunaingia mikataba na kampuni mbalimbali za utangazaji ili soka hiyo iweze kuonyeshwa live katika luninga zetu na hata kutangazwa katika redio mbalimbali.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kwa kuwa maeneo ya uchimbaji madini (mining sites) katika Mkoa wa Dodoma yako zaidi ya 700 na kuna baadhi ya maeneo hayajaanza kuchimbwa kabisa madini. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutangaza kwa wawekezaji ili kusudi waweze kuja kuchimba katika Mkoa wa Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi, tuna maombi mengi sana ambayo wachimbaji wadogo na wakubwa wameomba katika Wizara yetu kupitia Tume ya Madini. Hapa Dodoma kuna wachimbaji wadogo wadogo wengi wameomba leseni hizo, kwa maana ya kwamba wanataka au wameonesha nia ya kuchimba. Sisi kama Serikali hivi karibuni ile Tume imeshaanza kufanya kazi na zile leseni tutazitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema toka mwanzo kwamba tunataka tuwawezeshe wachimbaji wadogo. Mradi katika Wizara yetu ambao ni mradi unaopata fedha kutoka Word Bank, yaani Mradi wa SMRP; mradi huu tunaangalia namna bora sasa ya kuwawezesha wachimbaji wadogo, kwa maana ya kuwasaidia kuwapa teknolojia, elimu na mitaji ili waweze kuchimba. Pia wachimbaji wa Mkoa wa Dodoma na wao wamo kwa sababu sisi tunafanya kazi nchi nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa wachimbaji wadogo ambao wako katika Mkoa wa Dodoma, nipende tu kusema, walioonesha nia au walioomba maombi ya leseni, leseni zitatoka na wachimbaji ambao wanataka kuomba leseni sasa hivi Tume imeanza kufanya kazi walete maombi hayo katika Wizara yetu, tuweze kuwapa leseni, na tuangalie namna ya kuwasaidia ili waweze kuchimba na Wizara iko tayari na tunaendelea na kazi hiyo. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mkoa wa Dodoma ni miongoni ya mikoa yenye mifugo mingi sana ikiwemo ng’ombe na kuna nyakati wafugaji wanakosa soko. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhamasisha wadau na wawekezaji mbalimbali ili waweze kujenga Kiwanda cha Maziwa na collection centre katika Mkoa wa Dodoma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wetu ni kuhakikisha kwanza vile viwanda vyetu tulivyonavyo vinafanya kazi ya kuchakata mazao ya mifugo. Hapa Dodoma tunacho kiwanda kikubwa cha TMC ambacho hivi karibuni utendaji wake wa kazi haukuwa mzuri sana lakini Wizara tumeingilia kati tunahakikisha kwamba kiwanda chetu hiki kinafanya kazi nzuri ya uchakataji wa mazao ya mifugo kwa maana ya uchinjaji na hatimaye kutengeneza zile nyama kwa ajili hata ya kuuza nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali lake ni kujua namna tunavyoweza kuwavutia wawekezaji wa Kiwanda cha Maziwa hapa Dodoma. Nataka tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wana Dodoma wote kwamba ombi hili la kuhakikisha tunakuwa na Kiwanda cha Maziwa hapa Dodoma tunalichukua na tutahakikisha kwamba Dodoma na yenyewe pia inakuwa centre nzuri ya kuhakikisha tunatengeneza mazao ya mifungo ikiwemo maziwa na kuyasambaza kote katika nchi yetu.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza na namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake lakini nina maswali yangu mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa wananchi wengi hawafahamu waende wapi pale matatizo wanapohitaji unasihi na hii imejidhihirisha hivi karibuni baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kutangaza wanawake waliotelekezwa waende kwake, wamejitokeza wengi sana, sambamba na hilo na wanaume pia walijitokeza. Sasa nilitaka kufahamu je, Serikali haioni imefikia wakati wa kuhabarisha jamii kwamba huduma hizi zinatolewa ili waweze kupata huduma hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Maafisa Ustawi wa Jamii na Maafisa Maendeleo ya Jamii wako katika ngazi mbalimbali, je, Serikali haioni umuhimu wa kutenga siku maalum walau siku mbili kwa wiki na kutenga maeneo maalum ili wananchi waweze kwenda kupata ushauri wa unasihi badala ya kusubiri kwenda kipindi cha muda wa kazi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ni kuhusiana na suala la uelewa wa wananchi, tunapokea ushauri wake na tutaufanyia kazi kwa lengo la kujengea uelewa na nitoe rai tu kwa wananchi kwamba huduma za ustawi wa jamii zipo katika Halmashauri zote na katika baadhi ya maeneo hadi katika ngazi ya kata. Wanapokuwa na changamoto zinahusiana na masuala ya migogoro ya familia masuala ya ustawi, watoto yatima, waende katika ofisi za Halmashauri ama za ngazi ya kata kuweza kupata huduma hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili katika swali lake la nyongeza ameulizia kwamba kwa nini Serikali isitenge siku maalum na maeneo maalum ili huduma hii iweze kupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa Maafisa Ustawi wa Jamii ni waajiriwa wa Serikali na wapo muda wote kuweza kutoa huduma hizi kwa hiyo, huduma hizi zinatolewa siku zote za kazi katika muda wa masaa ya kazi katika maeneo husika ngazi ya Halmashauri, kata na mitaa ambapo Maafisa Ustawi wa Jamii wapo.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Kijiji cha Kwahemu, Kata ya Haneti, kuna vikundi 16 ambavyo vina wachimbaji zaidi ya 200 lakini havina maeneo ya kuchimba madini licha ya kupeleka maombi Tume ya Madini. Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu kuwapa maeneo wachimbaji hawa wadogo ili waweze kujikimu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli maeneo ya Kwahemu (Haneti), kuna uchimbaji mdogo mdogo wa madini ya vito. Katika eneo lile kuna leseni moja inamilikiwa na Bwana Dimitri, raia mmoja wa kigeni lakini kuna maeneo mengine ambayo yako katika utafiti kwa maana ya PL. Kama nilivyosema siku zilizopita ni kwamba tunafuatilia zile PL zote ambazo hazifanyiwi kazi tutazichukua na tutazifuta na tutawapa wachimbaji wadogo wadogo waweze kuchimba na waweze kujipatia riziki kama tulivyojipangia katika Serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge watu wa Kwahemu maeneo ya Haneti tuna mpango kabambe wa kuwapa maeneo ya kuchimba. Wale wachimbaji walioko pale nilishafika na wakatoa kero zao na mimi kwa kweli naendelea kuzifuatilia kwa maana ya kuzitatua na tunahakikisha kwamba hawa watu wa Kwahemu watapata leseni na wataweza kupata nafasi ya kuchimba.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa watoto hawa wadogo hawatumiki katika kubeba mizigo tu, lakini kuna wengine ambao hutumika kuwaongoza baadhi ya wazazi au walezi na watu wazima katika kwenda kuombaomba.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwanusuru watoto hawa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tumefanya sensa ya kubaini watoto ambao wanaishi mitaani au wanaoishi katika mazingira hatarishi katika baadhi ya Majiji na tumebaini idadi na wale ambao tuliwabaini na vyanzo vyao ambavyo vimewasababisha wao kuwa mitaani wengine tumeweza kuwaunganisha na wazazi wao, lakini vile vile, tunaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha kwamba wale ambao tunawabaini hawana wazazi kabisa, tunawatunza katika nyumba zetu za kuwalelea watoto.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatozo la mimba utotoni pia linawahusu sana watoto wenye ulemavu walio nje ya shule na ambao wako ndani ya shule. Je, Serikali inawanusuru vipi hawa watoto wenye ulemavu na mimba za utotoni?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu niliyotoa kuhusu watoto wa kike wanaokatishwa safari ya masomo kutokana na mimba, vilevile yanaweza yakatumika kwa ajili ya watoto walemavu kwa sababu tunachosema Wizara yetu na Serikali kwa ujumla inahakikisha kwamba hakuna mtoto yoyote wa Kitanzania atakayekosa elimu kwa sababu yoyote ile. Sisi tunachotaka ni ushirikiano kutoka kwa wazazi kwa sababu tayari Serikali ina mipango ya kuhakikisha kwamba yeyote yule anapata elimu bila kujali changamoto yoyote imempata katika safari yake.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pia namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Naibu Sika, wosia wa mdomo au wa matamshi una changamoto nyingi. Kwa kuwa mazingira ya ndugu au mashuhuda huweza kubadili wosia kwa mtoa wosia, sasa hivi tuko kwenye ulimwengu wa sayansi na teknolojia, je, kwa nini Serikali isifanye utaratibu wa kurekodi wosia wa mdomo na kuhifadhi RITA ili wanawake na watoto wasipoteze haki zao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa mujibu wa gharama za RITA kutunza wosia unatunza kulingana na mali aliyonayo mweka wosia ambayo ni kuanzia Sh.5,000 hadi Sh.50,000. Je, Serikali haioni umefikia wakati wa kufanya marejeo ya gharama hizo? Ahsante sana.
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa maswali ya nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge Kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumefikia kipindi cha utaalam wa kisayansi, nakubaliana na yeyee kwamba wosia usiwe tu wa mdomo, lakini tutumie njia ya kurekodi wosia huo kutoka kwa wazazi, kutoka kwa jamii. Pia nataka kumhakikishia kwamba Ofisi za RITA ziko katika kila Wilaya kwenye Ofisi ya DAS na tutajitahidi kama Serikali kuweza kuziwezesha kuwa na mashine za kurekodi wosia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka kumhakikishia kwamba kuna Mashirika mengi Yasiyo ya Kiserikali ambayo yamekuwa yanafanya kazi na jamii mbalimbali, kwanza kutoa elimu juu ya umuhimu wa kuweka wosia na pili jinsi ya kuandika wosia. Kwa hivyo Serikali yetu kwa kutumia sheria iliyopitishwa mwaka 2017 ya Misaada ya Sheria tutafanya pamoja ili kuhakikisha kwamba tunaboresha uandikaji wa wosia kwa wahusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, amesema sawa kwamba gharama kuanzia milioni 50, gharama ni Sh.5,000, kuanzia milioni 51 mpaka millioni 200 gharama za uandikishaji ni Sh.20,000. Kuanzia milioni 201 mpaka milioni 500 ni shilingi 30,000 na kuanzia hapo na kwenda juu ni shilingi 50,000. Ukitazama gharama hizi kwa kweli sio kubwa sana na kama tutapata mawazo kama uliyoyatoa hapo na kutoka kwa wananchi na kutoka kwenye ofisi zetu tunaweza tukatazama upya gharama hizi kulingana na mahitaji yatakavyojitokeza ili iwe ni motisha kwa wazazi, kwa ndugu kuweza kujiandikisha na kutumia huduma hii ya Serikali na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Ahsante.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo taarifa kuwa vituo vikubwa vinapima ulevi lakini kuna baadhi ya madereva wa magari makubwa wenye kuendesha masafa marefu wanavyopata muda wa kupumzika vituo vya njiani wanakesha wakinywa pombe na kusababisha ajali.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwadhibiti madereva hawa ili kupunguza ajali za barabarani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Dodoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ambazo tunachukua katika kudhibiti madereva walevi, likiwemo kusimamisha magari hasa haya ambayo amezungumza yanayobeba abiria na mizigo na kuwapima vilevi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa tukifanya kazi hiyo maeneo mbalimbali nchini na kwa kiwango kikubwa tumefanikiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa aina ya madereva ambao wanaendesha magari hali wakiwa wamelewa. Pale ambapo tunawabaini basi hatua za kisheria zinachukuliwa dhidi yao.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza, nina maswali mawili ya nyongeza. Naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake; lakini sambamba na hilo; kwa kuwa vituo vilivyopo katika haya maeneo havitoshelezi, hii imebainishakabisa katika majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, nilipenda kujua, je, serikali ina Mkakati wowote wa kujenga vituo vya nyongeza katika bajeti ya mwaka ujao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa taarifa za ukatili hasa ulawiti kwa watoto wa kiume zimekuwa zikiongezeka, na inawezekana ni kutokana na utandawazi; je, Serikali ina mkakati wowote wa kuzuia hizi picha mbaya au picha za ngono ili kuweza kunusuru kizazi hiki?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza sana amekuwa ni mdau mkubwa sana wa kufuatilia masuala mbalimbali yanayohusu afya ya mama na mtoto lakini vilevile masuala ya ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto, nikupongeze sana Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kusudio la Serikali kuongeza vituo hivi; kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kwamba tumeanza katika mikoa hii 11 na kusudio letu sisi kama Serikali nikufika katika mikoa yote. Ni kweli na ni lazima tukiri kwamba matokeo ya ukatili wa kijinsia yanazidi kuongeza ndani ya nchi yetu. Mwaka 2017 tulikuwa na matukio ya ukatili wa kijinsia takribani 41,000, mwaka 2018 yakawa zaidi ya 45,000 na sasa hivi tunafanya compilation ya matukio ya mwaka 2019. Lakini tunaamini kwamba matukio haya bado yanazidi kuongezeka na ndio maana sisi kama Serikali tumekuja na huu Mpango wa MTAKUWA ili kujaribu kuhakikisha tunadhibiti kabisa matukio haya, ikiwa pia na kwa kwenda sambamba na kuhakikisha kwamba wale wahanga wa ukatili wa kijinsia wanapata huduma stahiki. Kwa hiyo kusudio letu la Serikali ni kwenda katika ngazi zote, katika ngazi ya mkoa na baada ya hapo tutaanza kushuka katika ngazi ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili aliongea matukio ya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto hususan watoto wa kiume, na mligusia hili kutokana na masuala ya kiutandawazi. Ni kweli matukio haya tunayapata na sisi kama Serikali, na mara nyingi matukio haya yanafanywa na watu wa karibu ndani ya familia. Katika maelezo ya Mheshimiwa Waziri jana aliliongelea hapa ndani ya Bunge; kusema kwamba tunahitaji kwa kweli kama wazazi kuhakikisha tunakaa karibu zaidi na watoto wetu, tunafatilia maendeleo ya watoto wetu, tunakaa na kuongea na watoto wetu majumbani.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tuna mkakati mwingine wa ziada wa kuhakikisha kwamba katika shule tunaweka madawati ya masuala ya ukatili wa kijinsia; kwa sababu ukatili wa kijinsia mara nyingi unafanywa na watu wa karibu na nyumbani na saa nyingine mtoto anaweza asiseme kwa kuhofia kupata adhabu kwa mtu ambaye amemfanyia ule ukatili wa kijinsia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasahivi tunafanya maongezi na Wizara ya Elimu kuhakikisha kwamba kuna walimu katika kila shule ambao wamepata mafunzo haya ili watoto waweze kuyasema haya mashuleni na hawa walimu kuweza kusaidia kuchukua hatua. Vilevile tunashirikiana na Wizara ya Habari, Utamaduni na Sanaa kuhakikisha kwamba kunawekwa misingi mzuri ya udhibiti wa mtangazo katika redio, television na vyombo vingine vya habari kwa kuhakikisha kwamba zile content ambazo zipo zinaendana na maadili ya kwetu sisi kama Watanzania.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Dodoma – Kondoa – Babati ilifunguliwa mwaka 2018 na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini katika baadhi ya maeneo ya barabara hii kumeshaonekana uharibifu wa kuwa na mashimo na hivyo kuhatarisha usalama wa raia pamoja na magari: Je, Serikali inatoa tamko gani kwenye hii barabara mpya ambayo imeshaanza kupata uharibifu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yako maeneo ambayo yamekuwa dhaifu baada ya ujenzi wa barabara. Hata hivyo, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba barabara hii ya kutoka Dodoma - Kondoa – Babati ni kati ya barabara ambazo zipo kwenye kiwango kizuri na imejengwa kwa teknolojia mpya, hii ni super pave ukiilinganisha na barabara nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni kweli kwamba yako maeneo ambayo yamekuwa na upungufu. Vile vile uko utaratibu wa kimkataba kwamba kipindi cha matazamio barabara inafanyiwa urejeshaji. Kwa hiyo, tutaendelea kusimamia taratibu zilizokuwepo ili kuona maeneo ambayo yana upungufu yanafanyiwa marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mara baada ya miaka mitano ni utaratibu wetu wa kawaida kutenga fedha kwa ajili ya matengenezo ya mara kwa mara. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na ubora wa barabara hii, maeneo yote ambayo yana upungufu tutaendelea kuyasimamia ili kuhakikisha kwamba barabara inakuwa kwenye kiwango cha hali ya juu na wananchi wanapata huduma nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa wanufaika wengi wa TASAF ni wazee wasiojiweza na wanatoka katika maeneo ya pembezoni na inapofikia siku ya kupokea mafao, huwa wanafika pale katika maeneo ya vijiji kwa kutumia usafiri na usafiri huo wanalipia zile fedha za mafao. Je, Serikali haioni umefikia wakati wa kubaini wazee hawa wasiojiweza na kuweza kuwapelekea zile fedha katika maeneo yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, hapa wakati najibu maswali yangu ya msingi na ya nyongeza ya Mheshimiwa Badwel nimesema, mkakati mmoja wapo wa Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha tunaboresha, kwamba tutakuwa tunawalipa walengwa wote kwa njia za kielektroniki kwa maana ya kwamba tumegundua kwamba walengwa wengine walikuwa wanakatwa fedha zao bila ridhaa yao na wengine walikuwa wanadhurumiwa, ndiyo maana katika kuboresha, tumeamua kwamba tutakuwa tunawalipa kwa njia ya kielektroniki. Ahsante.
MHE. FATMA HASSAN TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Sambamba na hilo nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na mpango mzuri wa RITA kuwa ifikapo 2025 kwamba idadi ya watanzania wasiokuwa na vyeti itakuwa imepungua kwa kufikia 46.5% ambayo bado ni idadi kubwa. Je, Serikali haioni umuhimu wa kufanya kampeni maalum ya muda maalum ili kuhakikisha kwamba idadi ya watanzania wasiokuwa na vyeti vya kuzaliwa inapungua hadi kufikia 10%?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Serikali ina mpango wa kuanzisha usajili kwa kupitia njia ya mtandao, na baadhi ya wananchi wengi bado hawajui kutumia mtandao. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka kompyuta katika kila Tarafa hapa nchini ili wale wananchi ambao hawana uwezo wa kutumia mitandao hiyo wakaenda kujisajili katika maeneo ya Tarafa? (Makofi)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mbunge kwa kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Moja ikiwa inahusiana na kampeni ya kuwafikia watu waone umuhimu wa kuandikisha watoto kabla ya miaka mitano na kampeni ambayo sasa hivi tunaendelea nayo ya kusajili watoto waliozaidi ya miaka 15. Mbali na mfumo wa kuandikisha katika shule, kampeni zetu zinaendelea, RITA wanampango kwenye redio, wana mpango kwenye television na pia katika matukio mbalimbali ya kitaifa. Kuna vipeperushi ambavyo vinaeleza kila pale ambapo tuna nafasi, lakini pia tunashirikiana na mitandao mingine kama vile Uhamiaji na NIDA ili kupeleka taarifa hii hasa NIDA ambao ili kuandisha na kumpa mtu kitambulisho cha Taifa wanahitaji vyeti vya kuzaliwa.

Mheshimiwa Spika, mtandao huu tutautumia kwa makini, na tusaidiane na ninyi Wabunge katika hotuba zenu, katika mikutano yenu umuhimu wa kuwahamasisha wananchi wajiandikishe kwa kutumia ofisi zetu zilizoko kwenye Kata na kwenye Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, masuala ya kompyuta na mtandao, kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Spika kwa kutuelimisha na sisi Wabunge tuanze kutumia tablets na tunajifunza. Hii ni elimu endelevu kwa kuanzia hapa Bungeni ambayo lazima iwafikie wananchi, hatujauliza gharama za sisi hapa Wabunge kupewa tablets lakini kuna gharama. Itakuwa ni busara sana na wazo hili tunalichukua kuweza kufikisha vyombo hivi vya kompyuta siyo tu kwenye Serikali za Mitaa, lakini kufikisha mpaka kwenye Tarafa. Nashukuru Wizara ya Elimu ambayo sasa hivi imeingiza mfumo wa kufundisha kompyuta na matumizi ya IT.

Mheshimiwa Spika, suala hili ni changamoto kwa Taifa, nawaomba Wabunge kama kutakuwa katika bajeti za Wizara mbalimbali tukiomba fedha za kuleta mfumo wa Information Technology mtupitishie fedha hizo. Katika hili suala la uandikishaji naomba mtusaidie sana ili watu wa kawaida waweze kunufaika na kuwa na kompyuta. Siyo tu kwa ajili ya kuandikisha ili wapate vyeti, lakini kompyuta ni sawa na kujifunza kusoma na kuandika katika karne ya 21. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nimshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Pamoja na majibu hayo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Serikali kuanzisha programu mbalimbali lakini bado kuna tatizo la masoko. Je, Serikali ina mkakati gani sasa kuwasaidia vijana hawa katika upatikanaji wa masoko?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, vijana 32,563 waliopata mafunzo idadi yao ni ndogo sana ukilinganisha na vijana ambao wako maeneo mbalimbali vijijini.

Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kuongeza idadi ya vijana wengi zaidi, walau waweze kufikia hata asilimia 50 ili kusudi waweze kuacha kukimbilia mijini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA: Mheshimiwa Spika, nikianza na la kwanza kuhusu masoko; moja kati ya mpango ambao tunautekeleza ni mpango wa kuwashirikisha vijana kwenye kilimo ambao tunaufanya kwa pamoja na Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa vijana wanaofanya shughuli za kilimo hivi sasa kupitia maelekezo ambayo yalitolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa Mheshimiwa Waziri wa Nchi ambayo na mimi pia nimeshushiwa kwa ajili ya kuyatekeleza, hivi sasa tumeanzisha programu maalum ya kuanza kutafuta masoko ya bidhaa hasa bidhaa za kilimo za vijana wetu ambao wanafanya shughuli hizo kupitia viwanda vya ndani.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa tunatarajia kwenda kutengeneza shamba kubwa la mfano katika eneo la Mboga, Wilaya ya Bagamoyo ambapo kipo Kiwanda cha Sayona ambacho kimekubali kununua matunda kutoka kwa vikundi vya vijana ambao sisi tutawatayarishia mashamba, lakini vilevile pamoja na kuwatafutia mbegu pamoja na Wataalam wa SUA wameshafika katika eneo hilo. Kwa hiyo, katika upande wa kilimo tumeanza kuzungumza na viwanda na makampuni makubwa, ili pia iwe sehemu ya soko kwa bidhaa za vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kwa wale vijana ambao ni mafundi, wameunda makampuni, wanafanya shughuli mbalimbali za utoaji huduma, hivi sasa yalitoka maelekezo kwamba, kila Halmashauri nchi nzima itenge asilimia kadhaa ya manunuzi yake ya ndani kwa ajili ya vikundi hivi vya vijana. Na ninavyozungumza hivi vijana wengi wanaofanya shughuli za ufundi seremala ambao wanatengeneza madawati walipata kazi Halmashauri nyingi nchini kusambaza madawati, ikiwa pia ni sehemu ya soko, lakini pia kama Serikali tunaweka mpango mkakati mzuri kuhakikisha kwamba tunaweka mfumo endelevu wa vijana hawa kupata masoko ya uhakika. Hayo ni maeneo mawili tu ambayo nimeyatolea mfano.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ilikuwa ni kuhusu idadi ndogo ya vijana. Ofisi ya Waziri Mkuu inatekeleza Programu ya Ukuzaji Ujuzi nchini ambayo imeanza mwaka 2016 mpaka mwaka 2021 yenye lengo la kuwafikia takribani vijana milioni nne ifikapo mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, nilichokisema hapa ni component moja tu katika utekelezaji wa mradi huu, lakini tunawafikia vijana wengi na lengo letu ni kuwafikia vijana zaidi ya milioni nne ifikapo mwaka 2021.

Kwa hiyo, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ni kwamba tunafahamu vijana ni kundi kubwa, tunaendelea kuwafikia kwa kupitia programu mbalimbai, ili wote waweze kunufaika na urasimishaji ujuzi huo.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa ajali za barabarani zimekuwa zikisababisha vifo na kuacha baadhi ya familia katika mazingira magumu kwa kupoteza wategemezi na pia wengine kupata ulemavu wa kudumu. Je, wahanga hao hulipwa bima au fidia yoyote ili kuwapunguzia machungu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ajali za barabarani ziwe zimesababishwa na bodaboda, bajaji, baiskeli au magari zimekuwa zikisababisha vilema kwa wananchi au hata vifo na inapotokea yule aliyeathirika kama ni kifo ama majeruhi anatakiwa kupitia Shirika la Bima ambalo ile gari imekingwa katika ajali aweze kufuatilia na mpaka aweze kulipwa mafao yake ya bima. Kwa hiyo, hili ni suala la kisheria na ninaomba Watanzania wote wafuatilie bima zao pale ambapo ajali zinatokea na pia niwaelekeze Jeshi la Polisi wamekuwa wakiwasumbua baadhi ya wananchi katika kuwapatia document muhimu ikiwemo michoro ya ajali pamoja na document zingine ambazo Mashirika ya Bima yanazihitaji ili waweze kupata bima zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia bado Tanzania hapa Watanzania bado wanalalamika na hususani hawa bodaboda. Bodaboda hawa nilishatoa maelekezo kwa mujibu wa Ilani hii ya CCM, ibara ya nne kwamba Ilani hii ya CCM kwa makusudi kabisa CCM imeamua kupambana na umasikini, kwa makusudi kabisa CCM imeamua kutengeneza ajira na ikatamka hasa kwa vijana. Ni nia ya Serikali kuwalinda vijana hawa wanaopambana na umaskini na wanaotengeneza ajira. Nikaelekeza kuanzia siku ile ya bajeti hakuna bodaboda itakayokamatwa na askari wa usalama barabarani na kupelekwa kituoni kama bodaboda hiyo haipo kwenye makundi matatu yafuatayo narudia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kundi la kwanza ni bodaboda ambayo imehusika kwenye uhalifu itapelekwa kituoni; bodaboda kundi la pili ni ile ambayo haina mwenyewe imeokotwa, imetekelezwa itapatikana na kupelekwa kituoni; na kundi la tatu ni bodaboda ambayo yenyewe imehusika kwenye ajali ama ilikuwa imeibiwa imepatikana itakuwa kama kielelezo lakini makosa ya amebeba mshikaki, hana element, side mirror sijui imekuaje, wataendelea kupigwa adhabu zao na siku saba watatafuta faini bila bodaboda zao kupelekwa kituoni na nimesema tarehe 15 kama ambavyo imeandikwa kwenye Biblia kwamba siku ya kuja kwa mwana wa adamu mwana wa Mungu aliye hai hakuna ajuaye siku wala saa nitaanza kutembelea Vituo vya Polisi na ole wao nikute bodaboda hizi nilizokataza kwa nia njema ya CCM kwa watu wake zimewekwa kituoni, ahsante sana. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, maswali yangu ni haya yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, idadi ya wananchi 13,234 waliofikiwa pamoja na wadau wengine ni ndogo sana kulingana na idadi ya watu tuliopo katika nchi hii. Nataka kujua Serikali ina mkakati gani wa ziada wa kuwafikia wananchi ili kampeni hii iweze kufika katika eneo kubwa zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, naipongeza sana Serikali kwa kutekeleza Mpango Kazi wa Taifa wa kutokomeza ukatili pamoja na ndoa za utotoni. Hata hivyo, Mpango Kazi huu haufahamiki katika maeneo mengi na pia hata baadhi ya Wabunge hawaufahamu. Je, Serikali haioni umefikia wakati sasa kuishirikisha jamii katika kampeni hii ili kuwanusru watoto wetu wa kike? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fatma Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze amekuwa ni mdau mkubwa sana ambaye amekuwa anafuatilia haki mbalimbali na ustawi wa watoto wa kike pamoja na wanawake katika Mkoa wa Dodoma na Tanzania kwa ujumla. Nikupongeze sana Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na maswali yake mawili, la kwanza ni kuhusu idadi ndogo ambayo tumeweza kuifikia. Kama nilivyosema katika majibu yangu ya msingi, tulianza katika mikoa sita na tulijaribu kulenga maeneo ambayo tumekuwa na changamoto kubwa sana ya mimba za utotoni. Takwimu zetu za Kitaifa zinaonesha kwamba asilimia 27 ya mabinti kati ya miaka 15-19 aidha wana ujauzito au wameshazaa na Mkoa wa Katavi ndiyo unaongoza kwa takriban asilimia kama 49 na mikoa mingine ambayo tumekwenda kule katika kampeni yetu inaonesha kwamba ni ile mikoa ambayo kwa kweli ina mzigo mkubwa sana katika tatizo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejaribu sana kushirikisha makundi mbalimbali katika hili zoezi, siyo tu kwenda kuongea na jamii lakini tumejaribu kuangalia makundi gani ambayo yanaweza yakatusaidia kuweza kufikisha ujumbe. Tumeongea na viongozi wa kimila, kidini, Serikali, watu wa bodaboda, walimu na jamii kwa ujumla, lengo ni kuhakikisha kwamba ujumbe huu unafika vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tumekuwa tunatumia vyombo vya habari kwa kutumia televisheni, magazeti na majarida. Pia sasa hivi jambo lingine ambalo tumeanza kufanya ni matumizi ya sanaa katika kuhakikisha kwamba tunafikisha ujumbe. Tumeanza kufanya maongezi na wasanii mbalimbali ili na wao watusaidie kufikisha sauti zao kwa njia zao kwa makundi ambayo nao wanaongea nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili ambalo ameliulizia ni huu Mpango Kazi wa Serikali wa Kutokomeza Ukatili wa Kijinsia dhidi ya Wanawake na Watoto na mimba za utotoni. Sisi kama Serikali tumeshaanza mkakati wa kuhakikisha kwamba hizi Kamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto katika ngazi zote kuanzia ngazi ya Taifa mpaka ngazi ya vijiji zinatengenezwa na zinafanya kazi. Mpaka sasa hivi tuna Kamati takriban 10,000, tunaendelea kuziimarisha na kuzijengea uwezo ili nazo ziweze kwenda kusimamia majukumu haya ya kuhakikisha kwamba ukatili wa kijinsia ikiwa ni pamoja na mimba za utotoni unaondoka katika jamii yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa, tafiti zinaonesha kadri tunavyoendelea kuboresha elimu ndiyo hvivyo hivyo mabinti wanachelewa kupata ujauzito. Kwa hiyo, kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na Ofisi ya Rais (TAMISEMI) tutaendelea kuboresha mkakati wa kuonesha kwamba wasichana wote wanaendelea kukua shuleni ili kuanza kupunguza hili suala la ndoa na mimba za utotoni.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo :-
Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kufahamu Mradi wa SITETEREKI ulileta mafanikio kiasi gani wa kubadili mienendo ya vijana baada ya tathmini? Naipongeza Serikali kwa kuandaa ajenda ya Kitaifa ya afya kwa vijana na uwekezaji.

Je, utaratibu upoje katika kufanikisha elimu kwa vijana wenye Ulemavu wa akili kwani ni kundi ambalo lipo katika makundi yenye hatari kubwa ya kuathirika pia?
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, Mradi wa SITETEREKI ulianza 2018-2019 ambao ni mradi wa miaka mitano 2018/2023 ni jukwaa la vijana ambalo linatumika kuwafikishia ujumbe vijana kuhusu elimu ya afya ya uzazi. Jukwaa hilo, sehemu kubwa umekuwa ukifadhiliwa na USAID kupitia Mradi wa Tulonge Afya lakini kitaalamu Wizara ndio ilikuwa inatekeleza katika Mikoa 20 ya Tanzania Bara ambayo ilileta mafaniko ya kupunguza mimba za utotoni na kusimamia malengo ya kishule. Tathmini ya kati ya mradi itafanyika kuanzia mwezi Juni, 2020 na tathmini kubwa itafanyika mwaka 2023.

Mheshimiwa Spika, tumefanya rejea ya waelimisha rika (Pre Educators Manual) kwenye mapitio ya rejea hiyo tumeweka sura ya kuwafikia vijana wenye ulemavu ambapo tunategemea kuukamilisha hivi karibuni. Kwa kushirikiana na wadau wa Pathfinder na UMATI kuna Mtaala unaotengezwa ili kuwafikia vijana wenye ulemevu.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa tatizo lililopo katika Hospitali ya Mji wa Tunduma linafanana na Hospitali ya Uhuru iliyoko katika Wilaya ya Chamwino ya ukosefu wa wafanyakazi pamoja na ambulance na hospitali hii iko kwenye eneo ambalo ni la barabarani na linahitaji sana huduma za dharura kwa ajili ya wagonjwa.

Je, Serikali inatoa maelezo gani kuhusiana na upungufu huu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Uhuru inayojengwa katika eneo la Chamwino ni hospitali muhimu sana katika kuboresha huduma za afya katika eneo la Chamwino na Jiji la Dodoma kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali inatambua kwamba tunahitaji kupata kwanza watumishi wa kutosha katika hospitali ile kwa sababu ni mpya, ndiyo inakamilika na vilevile inatambua kwamba tunahitaji kupata vifaa tiba na gari la wagonjwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili tayari limewekwa kwenye mipango ya utekelezaji ya mwaka wa fedha ujao wa 2021/ 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimhakikishie kwamba tutakwenda kuhakikisha watumishi watakaoajiriwa watapelekwa katika Hospitali ile ya Uhuru. Tutakwenda kuhakikisha kwamba tunafanya utaratibu wa kupata gari la wagonjwa na vifaa tiba ili hospitali ile ianze kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana; namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake, lakini kwa kuwa Mheshimiwa Rais alishatoa ahadi wakati wa kampeni mwaka 2020 na Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza kwamba ni mradi wa kimkakati.

Je, kwa kuwa ilikuwa ni ahadi ya Rais, Serikali inatoa tamko gani kuhusiana na jambo hili? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi stendi ya Chema ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na ahadi zote za viongozi zinatekelezwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha na mipango inavyoandaliwa. Na katika jibu langu la msingi nimewaelekeza Halmashauri ya Chemba waandae andiko rasmi ambalo litawezesha sasa Serikali kuanza kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo wa kimkakati, lakini pia ambao pia ni ahadi ya viongozi wetu wa Kitaifa.

Kwa hiyo, niombe watekeleze utaratibu huo na Serikali iweze kuona namna ya kuanza kutekeleza mradi huu. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika eneo la Zuzu, Jiji la Dodoma kuna bonde kubwa sana ambalo linafaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Je, Serikali haioni umefikia wakati wa kuweka miundombinu katika bonde hili la Zuzu ili kusudi kuendeleza kilimo cha umwagiliaji?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mama Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, siyo tu eneo la Zuzu, Wizara ya Kilimo tutatumia potential area zote ambazo tunaweza kwanza kukusanya maji kwa ajili ya mabwawa ambayo yana gharama nafuu, lakini maeneo yote ambayo yana mabonde na yanatatusaidia katika eneo la umwagiliaji na hasa hii mikoa ya kati ambayo ina ukame lakini ina mvua za kipindi kifupi lakini nyingi.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Zuzu na maeneo mengine yote ambayo ni potential katika Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine tutaiweka katika mipango na tutaifanyia kazi.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Changamoto ya maji iliyopo katika Jimbo la Momba haitofautiani na changamoto iliyopo katika Jiji la Dodoma, kwamba kuna baadhi ya maeneo yamekuwa yakikosa maji hata kwa wiki tatu kwa maelezo kwamba mitambo ya Mzakwe imezimwa kutokana na ukosefu wa umeme.

Napenda kufahamu, je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na kadhia hii ili kuwaondolea wananchi usumbufu wa kukosa maji mara kwa mara. Ahsante.(Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Naibu wangu kwa kazi nzuri na namna gani anavyojibu maswali hapa Bungeni. Hata hivyo, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge, lakini kwanza nimpongeze Mama yangu Toufiq, kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya katika Mkoa huu wa Dodoma. Tukiri kabisa sisi kama Wizara ya Maji hapa Jiji la Dodoma kumekuwa na ongezeko kubwa la watu, uhitaji na uzalishaji wa maji katika Jiji la Dodoma uwezo wa mtambo wetu ni lita milioni 60 na mahitaji yake ni lita milioni 103 kutokana na ongezeko kubwa la watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa hiyo maelekezo mahususi ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa Wizara yetu ya Maji, kwa sababu lazima tumtue mwana mama ndoo kichwani. Tunakwenda kuyatoa maji ya Ziwa Victoria na kuja kuyaleta katika Jiji hili la Dodoma, ili kuhakikisha kwamba tunaondokana na changamoto hii. Kwa mkakati wa muda mfupi tunaendelea kuchimba visima virefu katika maeneo mbalimbali, ili kuongeza uzalishaji kwa muda mfupi na wananchi waendelee kupata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imekuwa ikisisitiza uanzishwaji wa vyama vya ushirika, je, Serikali haioni kwamba umefikia wakati kuwahamasisha wananchi wa Mkoa wa Dodoma wakaanzisha ushirika ukizingatia kwamba zao la zabibu ni zao la biashara na ni zao la kimkakati?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Dodoma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa mazao ambayo Serikali iliyaongeza katika mazao ya kimkakati ni pamoja na zabibu. Serikali inatambua umuhimu wa zao la zabibu katika Mkoa wa Dodoma na manufaa makubwa ambayo wananchi wamekuwa wakiyapata kupitia zabibu. Hivyo, katika kuharakisha maendeleo ya zao la zabibu katika Mkoa wa Dodoma hivi sasa tayari Mrajisi ameanza na zoezi la usajili wa Vyama vya Ushirika vya Msingi 11 na ifikapo mwishoni mwa mwezi huu wataitisha mkutano wa majadiliano kupitia kamati ambayo imeundwa kwa ajili ya kuja na Chama cha Ushirika ambacho kitasimamia vyama vya msingi, lengo letu ni kuendelea kuipa thamani zabibu ya Dodoma.

Mheshimiwa Spika, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba tayari mchakato umeanza na muda si mrefu tutakamilisha zoezi hili, na wakulima wa zabibu wa Dodoma watapata nafasi ya kuwa na chombo ambacho kitasimamia zao hili la zabibu katika Mkoa wa Dodoma.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ili nami niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo katika Halmashauri au Jimbo la Mbulu halitofautiani na tatizo lililopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa ambapo Daraja la Godegode halipitiki kwa muda mrefu sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nipate kauli ya Serikali kuhusiana na ujenzi wa daraja hili ambalo limekuwa ni kiungo katika kata za jirani lakini wananchi wamekuwa wakipata shida sana katika kupata usaifiri. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, daraja ambalo Mheshimiwa Mbunge amelieleza liko katika barabara ambayo inahudumiwa na TANROADS. Lakini kwa kuwa Serikali ni moja na sisi Ofisi ya Rais-TAMISEMI tunafanya kwa ukaribu sana na watu wa TANROADS tumelipokea hilo, na kwa sababu kama ni tathmini ya pamoja tunaifanya wote kwa pamoja, hususan katika zile barabara ambazo zina mwingiliano; kwa hiyo nilipokee na hili, nalo tuahidi tu kwamba tutalifanyia kazi ili kuhakikisha kuwa wananchi wa maeneo hayo wanapatiwa huduma. Ahsante sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nishukuru sana kwa majibu ya Serikali, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina swali moja la nyongeza.

Je, Serikali haioni imefikia wakati wa kutenga bajeti maalum ili kuweza kuwapeleka baadhi ya wataalam wa kilimo katika zile nchi ambazo zimekuwa zikizalisha zabibu kwa wingi ikiwemo Afrika ya Kusini, China na Spain? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawajengea uwezo wataalam wetu na hivi sasa tumekamilisha mazungumzo na wenzetu wa Afrika ya Kusini, Ufaransa na Israel kwa ajili ya kuwapeleka wataalam wetu kwenda kujifunza maeneo mbalimbali, ikiwepo ubunifu na uzalishaji wa mbegu bora na udhibiti wa magonjwa wa wadudu pamoja na mbinu bora za kilimo za shambani yaani agronomy.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Lahoda iliyopo Wilaya ya Chemba ina mnara ambao hauna nguvu, hivyo kuleta shida katika mawasiliano. Je, ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba wanaimarisha mawasiliano ili wananchi wa Kata hii waweze kupata mawasiliano? (Makofi)
NAIBU WAZIRI HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fatma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Chemba tayari tumeshatuma wataalamu wetu kwenda kuangalia changamoto iliyopo katika minara katika Jimbo la Chemba. Kikubwa tulichokuwa tunakiangalia ni aidha kuangalia kama kulikuwa na huduma ya 4G au haikuwepo, lakini kama ilikuwepo na changamoto ni mawasiliano hafifu basi tutahakikisha kwamba tunafanya namna ya kuongeza nguvu katika minara hiyo inayo lalamikiwa na wananchi. Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa idadi kubwa ya waathirika wa ukatili ni wanawake na watoto.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzuia idadi kubwa ya takwimu tunazoletewa hapa ili kupunguza ukatili huo? (Makofi)

Swali la pili, pamoja na kuwa Serikali imetoa taarifa kuwa wanaume 3,077 ndiyo waliofanyiwa ukatili wa kulawitiwa, sina shaka idadi kubwa itakuwa ni watoto wa kiume.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwalinda watoto wa kiume ili kusudi wasifanyiwe ukatili? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la takwimu linaweza kuonekana kwamba ni nyingi kwa sababu ya jitihada ambazo Serikali imechukua kupitia Jeshi la Polisi la kuanzisha Dawati la Kijinsia, ambapo hapo zamani watu wengi ilikuwa wanapata shida au wanaona aibu kuripoti matukio kama haya kwenye counter ya polisi. Kupitia uendeshwaji wa dawati hili watu wengi zaidi wamekuwa wakijitokeza na kutoa taarifa na hivyo basi kufanya sasa yale matukio ambayo hayatolewi taarifa zamani sasa yanaweza kutambulika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la mikakati ya kuwalinda. Suala la kuwalinda watoto wetu si jukumu la Serikali peke yake, hili ni suala la kila mmoja wetu tukianzia wazazi. Kwa hiyo, niseme wakati Serikali inafanya kila jitihada kuhakikisha kwamba inaweka mazingira mazuri ya ulinzi ikiwemo kuhakikisha kwamba inachukua hatua kali kwa wale wote ambao wanahusika na vitendo vya kuzalilisha Watoto wetu naomba sana wazazi na wenyewe wachukue majukumu yao ipasavyo, kwa maana ya kuangalia kuhakikisha wanafuatilia nyendo za watoto wao na kuhakikisha kwamba wanawalinda na kuwasimamia. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kuna kipindi kumekuwa kukitokea tatizo la upatikanaji mfumo hasa kwa watu wanaohitaji zile mashine za EFD, hivyo kuchelesha kupata zile mashine za EFD nini mkakati wa Serikali wa kuimarisha mfumo ili wafanyabiashara waweze kupata hizi mashine za EFD kwa wakati? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hizo zilikuwepo za mfumo huo wa mashine ya EFD na ndiyo maana tukaamua sasa kuleta mfumo mpya na kifaa kipya ambacho kinajulikana kwa VFD. Ahsante. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza. Niishukuru sana Serikali kwa majibu mazuri, nina maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwa na program maalum hasa kwa kutumia mapolisi kata ili waweze kutoa elimu kwa jamii kuweza kupunguza masuala ya ukatili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Kwa kuwa kuna baadhi ya wananchi wamekuwa wakisambaza picha ambazo zinaonesha matukio mbalimbali ya ukatili katika mitandao ya kijamii na picha nyingine zimekuwa zikikiuka haki za binadamu na kutweza utu wa wale ambao ni wahanga wa ukatili: Je, Serikali haioni upo umuhimu wa kuwa na namba maalum ya Serikali ambayo matukio yale yatapelekwa kule badala ya watu wachache kusambaza picha hizi katika mitandao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Fatma Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua umuhimu wa kuendelea kuimarisha elimu kwa ajili ya jamii nzima kupitia Polisi wetu wa Kata. Kwa kutambua hilo, ndiyo maana kuanzia mwaka 2022 Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imeridhia kutoa ajira zaidi ya Askari Wakaguzi Sasaidizi 3,200 na kupangiwa kwenye kata. Tumeanza kuona baadhi ya kata wameanza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Wabunge na viongozi wetu kwenye Wilaya na Halmashauri kuwatumia Polisi Kata hawa, hasa wanapokuwa na vikao vyao, mikutano ya hadhara ili waendelee kutoa elimu. Hii itasaidia kupunguza uhalifu kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juu ya ushauri alioutoa wa udhibiti wa usambazaji wa picha zinazokiuka haki na maadili, tunapokea ushauri huo ili tuweze kuufanyia kazi. Ni kweli, baadhi ya picha zinazooneshwa kwenye mitandao ya kijamii nyingine ziko vibaya sana, badala ya kusaidia zinaharibu kabisa. Kwa hiyo, tunaupokea ushauri huo ili tuweze kuufanyia kazi, ahsante sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante; nini mkakati wa Serikali wa kuzalisha zao la karanga ili kuweza kuchakata mafuta ya karanga na kupunguza uagizaji mafuta kutoka nje? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati mkubwa tulionao hivi sasa ni kuendelea kuisisitiza taasisi yetu ya kilimo (TARI) katika kuendelea kufanya utafiti na uzalishaji wa mbegu bora ili wakulima waweze kulima kwa tija na mwisho wa siku kama nchi tuweze kufikia malengo ya kuondokana na changamoto ya uagizaji wa mafuta.

Kwa hiyo, mazao ambayo tumeyapa kipaumbele katika kukamua mafuta ni pamoja na karanga, mchikichi pamoja na alizeti. Kwa hiyo, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge nisehemu ya mkakati wa Wizara.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, skimu ya umwagiliaji iliyopo katika eneo la Chikopelo Wilaya ya Bahi imeacha kufanya kazi kwa muda mrefu baada ya mwekezaji kuondoka. Nini kauli ya Serikali katika kuifufua skimu hii ili kuwaondolea umaskini wananchi wa eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunafahamu ya kwamba moja kati ya eneo ambalo litasaidia sana kukuza kilimo chetu katika nchi yetu ya Tanzania ni kilimo cha umwagiliaji. Namuahidi Mheshimiwa Mbunge ya kwamba Wizara tumejipanga kuhakikisha tunazipitia skimu zote ili kuweza kufahamu status zake kwa maana tujue ni miradi ipi haifanyi kazi, ipi inafanya kazi lakini ipi imekwamishwa na nini, ili tuitatue na kuwafanya wakulima wetu walime kilimo cha umwagiliaji. Moja wapo ya maeneo ambayo tutayapitia ni pamoja na eneo la Chikopelo.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wataalamu wa saikolojia na unasihi bado ni tatizo; je, Serikali haioni imefikia wakati wakaanza kliniki tembezi ili kuweza kutembea katika maeneo mbalimbali na kutoa huduma hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum wapo wataalamu hao katika kila mikoa na wanafanya kazi katika Halmashauri hadi vijijini. Pale wananchi ambapo wanapata tatizo katika vijiji vyao basi wamfuate mkuu wa Kijiji. Mkuu wa Kijiji atatoa taarifa katika Halmashauri kuhakikisha wataalamu wale wanakuja kuwapa elimu ya saikolojia watoto hao. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Nataka kufahamu nini mkakati wa Serikali wa kupeleka dawa za magonjwa yasiyoambukiza katika ngazi ya zahanati?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali moja ilikuwa ni kupatikana vile vitu ambavyo huduma hiyo inaweza ikafanyika na mmeona sasa hivi kwamba karibia kila jimbo kila mahali kuna ujenzi unaoendelea kwa ujenzi wa vituo vya afya, zahanati na mambo mengine. Kikubwa sasa hivi na kwa ajira iliyopo sasa hivi utaona sasa hivi Madaktari wenye level ya digrii sasa hivi wameshafikishwa mpaka vituo vya afya na dawa hizo zinaenda kutolewa kwa ukaribu zaidi. Kwa hiyo Serikali ina mkakati kuwa, tunapomaliza hivi vituo wakati tunaweka vifaa, tunaweka madawa, lakini wataalam watapelekwa wenye uwezo wa kuwatibu watu wenye matatizo hayo.
MHE. FATMA HASSAN TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa nchi yetu ina mifugo mingi ya kutosha, hivyo uwezekeno wa kuwa na mbolea ya samadi ni mkubwa, nini mkakati wa Serikali katika kuboresha na kuhamasisha matumizi ya mbolea ya samadi ili ilete tija? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa kwa hapa Dodoma tunacho kiwanda cha mbolea kinaitwa ITRACOM ambacho kinazalisha mbolea inayoitwa Organo Mineral ambapo zaidi ya asilimia 50 wanatumia samadi na imekuwa kichocheo kikubwa na soko la uhakika kwa wafugaji wetu wengi hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba ilikuwa ni mkakati wa Serikali, na kiwanda kipo hivi sasa na kinatumia malighafi hiyo kama sehemu ya kutengeneza mbolea hapa nchini.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, saratani ya kizazi pamoja na saratani ya matiti imekuwa ni tatizo kubwa sana kwa wanawake. Je, nini mkakati wa Serikali wa kufanya utafiti wa kina ili kujua chanzo cha saratani hii ili iweze kuzuiwa badala ya kutibu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ndiyo maana umesikia kuna kampeni zinazoendelea kule shuleni na kwingine kuhakikisha kwamba watoto wanapata chanjo hasa watoto wadogo na wasichana, vilevile tunahamasisha sana kupima.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachukua ushauri wako na tutaendelea kufanya utafiti na kuona changamoto zinazosababisha mambo haya yaongezeke kila siku.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa niombe radhi uliniita lakini sikuwa nimeuliza swali. Naomba niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa, kuna baadhi ya viwanda vinazalisha mbolea hapa nchini kikiwemo kiwanda cha Intracom pale Nara, kiwanda cha Minjingu na viwanda vinginevyo. Je, nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba viwanda hivi na vinginevyo vinazalisha mbolea ya kutosha ili kuweza kukabiliana na upungufu wa mbolea nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA
KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Dodoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali ni kuleta wawekezaji wengi nchini ili waweze kuzalisha mbolea ya kutosha kwa ajili ya kusaidia usambazaji wa mbolea kwa wakulima wote nchini, ndiyo maana ukiangalia moja ya mwekezaji wetu ni hawa Intracom kutoka Burundi ambao wao watazilisha karibu tani 60,000 na moja ya mkakati mwingine wa Serikali ni kuhakikisha Minjingu inaongeza uzalishaji kutoka tani 30,000 mpaka tani 100,000 kwa mwaka. Lengo ni kuahakikisha kwamba wakulima wanapata mbolea zote kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuondoe hofu huo ni mkakati wa Serikali na Serikali iko kazini kuhakikisha tunaongeza wawekezaji vilevile tunaongeza wigo wa viwanda vilivyopo kuongeza uzalishaji nchini. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Posta cha Dodoma ni kituo ambacho kimejengwa muda mrefu sana na hakiendani na hadhi ya makao makuu, nini mkakati wa Serikali wa kujenga kituo kipya cha posta cha kisasa ili kiendane na hadhi ya makao makuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA NA HABARI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Hassan Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumefanya ukarabati nchi nzima na kituo cha posta kikiwaki moja wapo. Pamoja na hivyo, tunaendelea na kutafuta maeneo ya kujenga vituo vingine vipya kulingana na Serikali kuingia makubaliano na Posta ya Oman. Tunaamini kabisa kwamba katika mradi huo ambao takribani milioni 100 USD zinaenda kutumika kujenga zile logistic park. Naamini kwamba kwa sababu Dodoma ndiyo makao makuu ya nchi tutaitazama na kuhakikisha kwamba inakuwa na posta ya kisasa na yenye kutoa huduma ambazo zinaendana na mahitaji ya Watanzania.
MHE. FATUMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Eneo la Nkuhungu katika Jiji la Dodoma ni miongoni mwa maeneo ambayo yanaathiriwa sana na mafuriko mara kwa mara. Nini mkakati wa Serikali wa kutengeneza miundombinu mizuri ili kuwanusuru na mafuriko wananchi hawa wa eneo la Nkuhungu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo maeneo ambayo hali iliyofikia sasa hakuna namna nyingine isipokuwa ni kutengenezewa miundombinu ambayo itakwenda kudhibiti hii hali na kuwaacha wananchi wakiwa salama. Nimwambie Mheshimiwa kwanza tutataka tufanye study, tufanye utaratibu maalum wa kufanya tafiti kujua nini kinatakiwa hapo, kama ni daraja au ni kivuko kingine chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili, tutafute fedha sasa, kwa sababu hivi vitu vinataka fedha. Nimwambie Mbunge awe na Subira, maeneo yote ambayo yanaelekea ama yameshaingiliwa na maji na yanasababisha mafuriko hasa kipindi cha mvua kubwa, Serikali kwa kupitia ofisi yetu itahakikisha kwamba tunayashughulikia, nakushukuru. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Msingi Kizota ambayo iko katika Jiji la Dodoma ni miongoni mwa shule ambazo zina wanafunzi wengi sana na hivyo kusababisha wanafunzi kuingia kwa zamu.

Nini mkakati wa Serikali wa kujenga shule katika eneo la mnada mpya ambapo hakuna shule kabisa kwa sababu watoto wengi wanatokea eneo lile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari kujenga shule nyingi kwa wakazi wa kule Kizota kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mradi huu wa BOOST ambao Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashuhuda, fedha nyingi sana imetolewa na Serikali hii ya awamu ya Sita kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa shule tuone ni namna gani tunaweza tukafanya kwa ajili ya wakazi wa Kizota wapate shule nyingine na wanafunzi waache kwenda kwa zamu pale.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Kumekuwa na Waganga wa Jadi na wa Asili ambao wamekuwa wakibaini kwamba wao wanatibu kansa mbalimbali: Nini kauli ya Serikali kuhusiana na waganga hao ambao wamekuwa wakiwapa wagonjwa taarifa ambazo siyo sahihi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, kauli yetu ni moja tu kwamba, yeyote atakayeibuka akiwa na jambo hilo, moja, tunatuma watu wetu wa Mkemia Mkuu, lakini taasisi ya tiba asili kuhakikisha na kukiangalia kile anachokisema kama ni kweli. Tunapogundua siyo tiba, tunamzuia kufanya hivyo na tunamtia moyo wa kuendelea kufanya utafiti na kufikiria namna ya kutatua kwa pamoja kwa kushirikiana na sisi. (Makofi)
MHE. FATMA TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Waathirika wakuu wa suala zima la tabianchi ni wanawake na hasa wale wanawake wanaoishi maeneo ya pembezoni. Nini mkakati wa Serikali wa kuwa na program maalum kwa ajili ya hawa wanawake wa pembezoni waweze kupata mafunzo kukabiliana na hali ya tabianchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, tayari alichokiomba Mheshimiwa Toufiq tumeshakianza. Tumeanza na Mkoa wa Kaskazini Unguja, tayari kule viko vikundi vya akinamama vya ujasiriamali katika Jimbo la Chaani. Tumeshaanza hiyo program ya kuwapa taaluma akinamama ili waweze kujua namna bora ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Haya tumeyafanya kwa sababu, tumeona baadhi ya shughuli za uvuvi, lakini hata shughuli za ulimaji na uvunaji wa mwani, wengi wao tumegundua ni akinamama. Kwa hiyo, tumeona tuendelee kuwapa hii elimu ili waweze kuepukana na hizi athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Nini mkakati wa Serikali wa kuhamasisha wanawake wengi zaidi wafuge kwa kutumia vizimba ili wawezekuepukana na umasikini? (Makofi)

NAIBU WAZIRI MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Jambo la kwanza, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inazingatia sana na imekuwa ikihimiza wanawake kujiunga katika ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba. Ndiyo maana sasa hivi katika kila programu ambayo tunaianzisha tumeweka pale threshold ambayo lazima kwenye kila program pawepo na wanawake wanaojiunga na shughuli hizo. Kwa hiyo, hiyo ni sehemu yetu na tutaendelea kuisimamia kuhakikisha kwamba wanawake wanaingia katika shughuli hizi, ahsante sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Baadhi ya wahanga wa ukatili wamekuwa wakirushwa picha zao katika mitandao hivyo kutwezwa utu wao; na hivyo kusababisha baadhi ya ambao wanafanyiwa ukatili kutokutoa taarifa: Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na jambo hili?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq kuhusu hao wanaopiga picha mitandaoni, kweli inasikitisha sana. Serikali imekuwa ikitoa maelekezo na maagizo ya kwamba waache kufanya hivyo, na wamekuwa wakiendelea. Sasa kauli ya Serikali ni kwamba, vitendo hivyo ni vibaya katika malezi, makuzi na maadili ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vitendo hivyo vinawaharibu watoto wetu ambao ni Taifa la kesho. Kwa sababu wamekuwa hawasikii, sasa hili ni onyo la mwisho, vinginevyo nakwenda kuita kikao cha wadau wote na wote hao waliopiga hizo picha za namna hiyo, nitaongoza kwenda kuwashitaki kwa mujibu wa sheria kwenye Jeshi la Polisi ili sheria zetu tulizozitunga wenyewe zifanye kazi yake, zisikae tu kabatini. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Je, Serikali ina mkakati gani wa kubaini mila zote nzuri ili kurithisha vijana wetu wa sasa waachane na mambo ya kigeni?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa nchini Tanzania tunazo mila nyingi sana nzuri ambazo kwa wakati wa sasa zingetusaidia kupambana na mabadiliko ya mmomonyoko wa maadili katika dunia nzima jinsi ambavyo inakumbwa. Hivyo basi, nimepokea hoja hii, tutakwenda kuunda kikosi kazi tukishirikiana na Wizara ya Utamaduni, Michezo na Sanaa pamoja na Wizara nyingine zote tuweze kuja na list ya hizo mila nzuri, kwa pamoja tuweze kuweka mkakati wa kuzielimisha, kuzithibitisha na kuziweka kwenye kumbukumbu sahihi za mila zetu ambazo tutakuwa tunazifanyia kazi Nchini.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina swali moja la nyongeza. Je, Serikali haioni umefikia wakati wa kuhamasisha wawekezaji wa ndani ili kusudi waweze kuzalisha mafuta yanayotokana na alizeti, ufuta, karanga, pamba, pamoja na mafuta yanayotokana na mifugo?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ni kweli moja ya maeneo ambayo Serikali imeweka kipaumbele ni kuhamasisha uzalishaji wa mafuta kwa wazalishaji wa ndani, pamoja na kukaribisha wawekezaji kutoka nje, lakini mkakati mkubwa ni kwa wazalishaji wa ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili tunalifanya kupitia, mosi kama nilivyosema, kuwawezesha wakulima ili kulima mbegu zenye ubora na zenye tija. Pili, tunatengeneza teknolojia rahisi, viwanda vidogovidogo ambavyo vitapelekea wananchi hawa wazalishaji wa ndani kuzalisha mafuta mengi, lakini yenye ubora kwa sababu, changamoto hapa si tu upatikanaji wa mafuta, lakini pia tunataka mafuta yenye ubora ambayo yatakuwa hayana athari hasi kwa walaji. Kwa hiyo, tunaendelea kuhakikisha tunawezesha teknolojia rahisi ili kuzalisha zaidi mafuta ya kula hapa nchini.
MHE FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Jiji la Dodoma limekuwa lina matatizo sana ya upatikanaji wa maji na hivyo kuwa kero kubwa sana kwa wananchi. Je, ni nini mkakati wa Serikali wa kupunguza tatizo hili ili kusudi wananchi waweze kufaidika na maji safi?

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Dodoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali kwa Jiji la Dodoma Waheshimiwa Wabunge naamini ni mashahidi tunaendelea kufanya kazi nyingi sana kuona tunakwenda kukomesha tatizo la maji katika Jiji la Dodoma kwa umuhimu wake kama Makao Makuu ya Nchi tuna miradi mingi mikubwa, ya kati na midogo, tunatarajia mwaka ujao wa fedha miradi mingi itaanza kupeleka huduma ya maji maeneo yote ambayo yanapata changamoto.

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa likizo ya uzazi ambapo wanaume wanapata siku tatu;

Je, Serikali haioni umefikia wakati kuongeza walau mwezi mmoja kwa wale wenza ambao watakuwa wamezaa watoto njiti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza lililoulizwa na Mheshimiwa Toufiq Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake linaweza kuwa limejibiwa vizuri sana na Mheshimiwa Waziri wakati anatoa maelezo ya ziada katika majibu yangu niliyompa Mheshimiwa Mtanda. Na mimi nadhani ili nalo tuliunganishe katika maombi aliyotoa Mheshimiwa Waziri la kutoa maoni ili kuona kama kuna sababu ya kurekebisha baadi ya vifungu vilivyomo katika sheria na kanuni inayoongozwa masuala yote ya likizo hasa pia kwa wanaume ambao Mheshimiwa Toufiq anawapigia debe waongezwe zifike siku 30. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mtaa wa Mpamaa ambao uko Kata ya Miyuji katika Jiji la Dodoma wananchi wamejenga zahanati, lakini hadi sasa zahanati ile haifanyi kazi. Nini kauli ya Serikali katika kuifanya zahanati hii ifanye kazi ili wananchi wapate huduma ya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ameainisha eneo la Mpamaa kwamba kuna zahanati ambayo imejengwa na bado haijafanya kazi. Nitoe kauli ya jumla kwa Serikali kwamba maeneo yote ambayo zahanati zimekamilika tungeomba tupate taarifa, ziletwe Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kufanya tathmini ya jumla kwa ajili ya usajili, vifaa tiba pamoja na wauguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Wanawake wengi sasa hivi wameanza kujiingiza katika biashara ya madini: Nini mkakati wa Serikali katika kuendeleza wanawake hawa kwa kuwapatia mikopo na kuwahamasisha wanawake wengi zaidi waweze kushiriki katika biashara ya madini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikubali kwamba katika watu ambao wamechangamkia fursa ya uchimbaji madini, kundi kubwa la wakina mama wameingia kwenye uchimbaji madini. Mahali ambako wanawake wanachimba, tuna uzoefu, ni watu waaminifu, wanaolipa kodi kwa wakati, hawahitaji kusimamiwa na Polisi; na hata mirabaha ambayo tumewapa kusimamia, wao wameonesha bila shaka yoyote kwamba ni watu wanaoweza kujisimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi Serikali tunaangalia utaratibu bora zaidi wa kuwapatia wachimbaji mikopo wakiwemo na wanawake. Tunachohitaji ni muda wa kufanya study. Kwa sababu kinachowekwa kama dhamana ya kuchukulia mkopo, tungetamani iwe hiyo leseni yenyewe ambayo mchimbaji anapewa. Kwa hiyo, tunalikamilisha ili tufanye kwa namna ambayo hatutakosea kama tulivyowahi kukosea huko nyuma, kuwapatia watu mikopo na baadaye watu hao wakapotea na fedha zenyewe.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Ugunduzi na ubunifu ni miongoni mwa nyanja muhimu sana katika ukuzaji uchumi na maendeleo. Nini mkakati wa Serikali katika kuendeleza ugunduzi na ubunifu katika nyanja za vijijini na hasa kwa wanawake?

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya msingi kwamba, kwanza tuna sera ya namna gani ubunifu na ugunduzi unasimamiwa au unaratibiwa katika maeneo yote. Katika kulisimamia hilo, Serikali baada ya kuona hii sera mwaka 2018 tumeandaa mwongozo wa namna gani masuala haya ya ubunifu yanaweza kusimamiwa na kuratibiwa kuanzia ngazi ya vijiji, kata, Tarafa, Wilaya, mpaka kufika katika ngazi ya Taifa ambako huko watu wote tunaweza tukawakuta.

Mheshimiwa Spika, ukitaka kuangalia kwa umakini kabisa katika mashindano yetu haya ya MAKISATU yameweza kubeba makundi yote, kuna makundi karibu saba tumeweza kuyazingatia tunapokwenda kuwagundua wagunduzi wetu au watafiti wetu katika maeneo yote ya vijijini mpaka katika ngazi ya Taifa. Kwa hiyo, katika eneo hili na wanawake vilevile wanaingia kwa namna moja au nyingine.

Mheshimiwa Spika, Nakushukuru sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini sambamba na hilo nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; naomba kupata commitment ya Serikali kuhusiana na kutunga sheria hii. Je, sheria hii itaweza kutungwa ndani ya uhai wa Bunge hili?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa, sheria imechukua muda mrefu kutungwa. Je, Serikali haioni sababu ya kutengeneza mkakati au mpango maalum wa kuona jinsi ya kuweza kuwaangalia hawa Maafisa Ustawi ambao wanakiuka taratibu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, inaona umuhimu wa sheria hii. Kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi Serikali itasimamia sheria hii ili iweze kuwasilishwa mapema katika Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili kuhusu Maafisa Ustawi kuwa na maadili. Ushauri umepokelewa. Hata hivyo, Wizara inafuata kanuni za utumishi wa umma kwa wafanyakazi wote na wafanyakazi wote wanaokiuka maadili, hatua za kisheria zinachukuliwa pale wanapofanya makosa. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna wanafunzi wa Shule za Sekondari ambao wamekuwa wakimaliza shule na wanazaidi ya miaka 18. Je, nini mkakati wa Serikali kutoa elimu katika shule mbalimbali ili wanafunzi wanapomaliza waliozaidi ya miaka 18 waweze kupata vitambulisho?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba baadhi ya wanafunzi huitimu masomo yao wakiwa na zaidi ya miaka 18 na wanafunzi wa aina hii wana haki ya kupewa vitambulisho. Kwa hiyo, pengine tutashirikiana na Wizara ya Elimu na Wizara ya TAMISEMI ili elimu ya uraia ikiwa ni pamoja na nafasi ya kuwa na vitambulisho kutolewa mashuleni, lakini wanafunzi hawa ni sehemu ya jamii kule ambako elimu inatolewa kwenye jamii kwa ujumla wake kupitia redio, televisheni na kadhalika wanaweza pia wakapata elimu hiyo. Kwa hiyo, nadhani halitakuwa tatizo kubwa sana litatekelezwa. Nashukuru sana.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumezuka vikundi vya wahalifu katika Kata ya Makulu, Jiji la Dodoma vinavyojiita panya karowa. Nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba vikundi hivi haviendelei katika maeneo mengine na kuleta uhalifu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tunapiga vita makundi yote ya wahalifu awe mtu mmoja au vikundi kama ilivyokuwa panya road Dar es Salaam. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa Dodoma hiyo kazi pia imeanza na baadhi ya vijana wa aina hiyo wameshatiwa nguvuni. Sasa hilo ulilosema eneo gani umetaja Kata ya hawa panya nini karoga? Tutashughulika nao hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kikao hiki tutaongea na Mbunge ili anieleze kwa ufasaha ni eneo gani na kundi hili ili askari wetu wa Jiji la Dodoma waweze kushughulika nao. Nashukuru. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali inatoa tamko gani kwa wale maaskari wapiganaji waliopigana Vita vya Kagera ambao hawakuajiriwa na sasa wana maisha duni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, ni kwamba kwa mujibu wa takwimu tulizonazo, wazee wote ambao wanapata huduma ya pension na usaidizi wa kimatibabu ni 272. Kama wapo wazee ambao kwa bahati mbaya hawakuingia kwenye orodha hiyo, tumeelekeza waende karibu na vikosi vya Jeshi vilivyoko jirani na makazi waliyopo ili taarifa zao zihakikiwe na hatimaye waweze kupata huduma kama zile wanazopata wazee wenzao waliopigana vita hii, ahsante.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu ya Serikali. Pamoja na majibu hayo, nina maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali inawachukulia hatua gani waajiri wale ambao hawawapi safari hawa wanawake wanaonyonyesha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, je, Serikali haioni imefikia wakati wa kuwa na takwimu sahihi ya wanawake wanaonyonyesha ili kupanga bajeti kuepukana na kisingizio cha ufinyu wa bajeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hatua gani zimechukuliwa na Serikali, nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako kwamba hatua zimeendelewa kuchukuliwa kwa waajiri wote ambao hawatekelezi majukumu kwa mujibu wa sheria tulizoziweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu takwimu, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba takwimu tumeendelea kuzichukua na kama zipo kesi zozote zile ambazo sisi kama Serikali hatuzifahamu au yeye kama Mbunge anazifahamu, basi ofisi yangu ipo wazi nakaribisha malalamiko hayo ili tuweze kuyashughulikia mara moja. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali la nyongeza. Nilipenda kufahamu: Nini mkakati wa Serikali wa kuwaandaa makocha wengi wanawake ili waweze kufanya ukocha hapa nchini na nje ya nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikakati tuliyonayo pia ni kuhakikisha kwenye ile michezo yetu ya kipaumbele kwa Wizara ambayo tuna michezo sita ya kipaumbele kwa Taifa ni pamoja na kuhakikisha pia tunapata makocha wanawake. Kwa hiyo, jambo hili Mheshimiwa Toufiq tunalizingatia pia.