Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Eng. Ramo Matala Makani (128 total)

MHE. RISALA S. KABONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini vilevile nilikuwa na maswali ya nyongeza.
Kwa kuwa Serikali kupitia mradi wa UNDP na USAID umepata Dola za Kimarekani 100,000 kwa ajili ya kufanya ukarabati mbalimbali kwa maeneo ya utalii; inaonekana kwamba Serikali imejipanga kukarabati uwanja wa Songwe, Katavi, Kigoma na Mpanda:-
Je, kwa kuwa mwaka 2009 Iringa iliteuliwa kuwa kitovu cha utalii, Serikali imejipangaje kuwekeza uwanja wa Nduli - Iringa ambao umekuwa na gharama kubwa sana za usafiri kuanzia Dola 180 mpaka Dola 200 kwa safari sawa na shilingi 400,000/= kutoka Iringa mpaka Dar es Salaam, Serikali imejipangaje kuwekeza katika uwanja huu? (Makofi)
Swali la pili; kwa kuwa Serikali imejipanga kuwekeza kwenye mahoteli, Serikali imejipangaje kutathmini viwango vya mahoteli ambavyo viko katika nchi hii, ukizingatia kwamba zoezi hili limefanyika baada ya uhuru; Mikoa ya Pwani, Dar es Salaam na Mikoa ya Manyara kwa kuweka madaraja ya nyota katika mahoteli? Ni eneo ambalo tunapoteza mapato sana na mahoteli mengi yanalipa kodi kutokulingana na nyota. Kwa mfano, hoteli ya nyota moja, nyota mbili, nyota tatu.
MHE. RISALA S. KABONGO: Je, Serikali imewekezaje katika upande huo?
Sambamba na hilo, Serikali imejipangaje kuboresha barabara ya kuelekea hifadhi ya Ruaha yenye kilomita 130 ambayo ina hali mbaya sana na kusababisha gharama za utalii kuwa kubwa katika Mikoa hii ya Nyanda za Juu Kusini hususan Hifadhi ya Ruaha ambayo ndiyo hifadhi kubwa kuliko zote Tanzania? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kuhusu namna ambavyo Serikali imejipanga kuweza kuboresha uwanja wa ndege wa Iringa kwa sababu ambazo nilizisoma na ambazo na yeye amezirudia.
Kwanza, ni nia ya Serikali kuendelea kufanya utalii kuwa chanzo kikubwa cha mapato kwa Taifa hili. Kwa sababu hiyo, ili tuweze kufikia lengo hilo, lolote linaloweza kufanya Serikali ikafanya vizuri zaidi kwenye Sekta ya Utalii ni kipaumbele katika Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, basi nilipotaja viwanja vya ndege na barabara na miundombinu mingine inayoboreshwa chini ya mradi huu ambao una ufadhili wa Dola milioni 100, huu ni mradi mmoja tu peke yake na jibu lililotolewa lilikusudia kujibu swali lililotolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema tu kwa ujumla, Serikali inajipanga zaidi kutafuta miradi mingine zaidi na kutafuta fedha zaidi ili kuweza kuboresha maeneo yote ambayo yatachangia katika kuboresha Sekta ya Utalii kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kutathmini viwango vya mahoteli, ameuliza swali ambalo sasa hivi liko mezani tayari na ninamshukuru Mbunge kwa mawazo haya mazuri ambayo yanaendana na jitihada za Serikali ambazo tayari zimekwishaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatutafanya tu zoezi la kupanga hoteli kwenye madaraja, bali pia ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba tunatoa elimu na kusimamia wawekezaji wa Kitanzania waweze kufikia viwango hivyo. Hoteli nyingi za sasa hivi zilizopo, hata kabla hujaenda kuzipa madaraja, nyingi zinahitaji kufanyiwa kazi ili ziweze ziboreshe huduma ili kuweza kuwafanya watalii waweze kujisikia kwamba wamekaa kwenye hoteli.
Kwa hiyo, kwanza tutaanza kutoa elimu na hapa nitoe wito, wote wanaokusudia kuwekeza kwenye eneo hili, waweze kuwasiliana na Idara ya Utalii kwenye Wizara hii, pale ambapo watahitaji; au wanaweza kupata utaalam kutoka mahali pengine, lakini wote tuwe na nia ya kuweza kuboresha huduma za hoteli ili wageni wanapokuja waweze kujisikia kwamba wako mahali penye sifa zinazotakiwa na viwango.
Kwa hiyo, tunakusudia kuanza hivi karibu kupanga hoteli zote katika madaraja katika Mikoa yote, siyo tu kwa ajili ya kuboresha mapato ya Serikali lakini pia katika kuwafanya watalii waweze kupata huduma zinazostahili.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu ya Serikali ambayo wananchi wa Busekelo hawajaridhika nayo, kwa sababu wananchi hawa wako pale tangu miaka ya 1950 na mipaka imefanyika mwaka 2006/20007, ni mwaka wa tisa sasa bado wananyanyaswa sana na watu wa TANAPA.
Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na watumishi wa TANAPA ambao wanawanyanyasa wananchi na wanashindwa hata kuendeleza maeneo yao ya kilimo, shule pamoja na makanisa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, atakuwa tayari tuongozane twende akajionee kuanzia mwanzo mpaka mwisho wa Bonde la Mwakaleli ili ukajithibitishe hiyo mipaka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASISILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, askari wanaosimamia utekelezaji wa sheria upande wa misitu na wanyamapori, wanaosimamia hifadhi walio wengi wanajitahidi kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria. Hata hivyo, kwa wale wachache ambao wanafanya hayo yaliyotajwa na Mheshimiwa Mbunge ya unyanyasaji na tabia nyingine zozote ambazo si nzuri, zinazoipaka matope Serikali wanafanya makosa na tunaomba pale ambapo inajitokeza, wanaohusika watolewe taarifa katika vyombo vinavyohusika watachukuliwa hatua zinazohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwenda, niko tayari kati ya Mkutano huu na Mkutano ujao, hebu tukutane baadaye tuweze kupanga vizuri ratiba, tunaweza kwenda wote kuangalia na kupata ufumbuzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni kwamba, Serikali imejipanga sasa na kwa sababu matatizo haya ni ya muda mrefu, sasa tumejipanga vyema zaidi na katika kipindi cha muda mfupi ujao mtashuhudia tunavyoweza kurudia kuweka mipaka kwa namna kabisa ya maelewano ya wale tunaopakana nao ili baada ya kuwa tumeshaweka mipaka hiyo, tunatarajia wananchi wataheshimu mipaka hiyo na wataacha kuvuka mipaka hiyo kwenda kwenye maeneo ya hifadhi.
MHE. HAROON M. PIRMOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu lake la msingi Mheshimiwa Waziri amesema Serikali iliunda timu ya wataalam kupitia upya mipaka iliyotangazwa ili kutoa mapendekezo kuhusu mipaka hiyo ya GN. Na. 28. Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba zoezi hili litamalizika lini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa mgombea Urais kupitia CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana aliwaahidi wananchi wa Mbarali wanaoishi katika vijiji hivyo 21 kumaliza kero hiyo na kwa kuwa mgombea huyo sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Je, Mheshimiwa Waziri kuendelea kuchelea kutoa jibu hili haoni kama anapinga ahadi aliyotoa Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ni lini au ni baada ya muda gani zoezi hilo ambalo linakamilishwa na Kamati iliyoundwa litakamilika? Nimepitia taarifa ya awali ya Kamati hiyo ambayo tumesema inakamilisha kazi iliyopewa, napenda kukufahamisha kwamba kazi hiyo ndani ya kipindi cha mwezi mmoja itakuwa imekamilika ikiwa ni pamoja na kwenda kufanya ukaguzi wa maeneo yanayohusika.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, pengine jambo muhimu si kuzungumzia zaidi kwamba kuna ukiukwaji au kuna utaratibu ambao unaonekana kupingana na ahadi aliyoitoa Mheshimiwa Rais, jambo la msingi hapa ni kwamba kazi hii ni muhimu na suala la kushughulikia changamoto za wananchi pia ni ahadi ya Serikali hii ya Awamu ya Tano na katika kipindi hicho ambacho nimekisema suala hilo litakuwa limekamilika na kupatiwa uvumbuzi.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Misitu Namba 14 ya mwaka 2002, ilizuia usafirishaji wa mazao ya misitu ambayo hayajachakatwa ikiwemo asali, mbao na hata wanyamapori. Naomba kuuliza swali langu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya zuio hilo Serikali imeruhusu kusafirisha mbao ya sentimita 15 tu unene na wakati huo wadau na masoko yanahitaji zaidi ya sentimita 15. Je, Serikali iko tayari sasa kuwaruhusu wafanyabiashara ambao wanafanya export ya mbao hizi, wakiwemo wafanyabiashara wa mitiki, pine na mbao za miche ya asili angalau wafikie katika sentimita 20 ili nao wapate tija na kushindana na wafanyabiashara wenzao katika masoko?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika Jimbo langu la Manyoni Magharibi na Wilaya nzima ya Manyoni, imezuia uvunaji wa mbao na mazao ya misitu kwa ujumla, Je, Serikali sasa ipo tayari kushirikiana na Halmashauri yangu mpya ya Itigi uvunaji uendelee, badala ya watu sasa kuiba ili walipe kodi za Serikali na maduhuli na pia kusaidia pato la Halmashauri wakati misitu ipo?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ambayo ameitaja Sheria Namba 14 ya mwaka 2002, Serikali iliweka utaratibu kwa uvunaji wa mazao mbalimbali ya misitu kama alivyoyataja na kwa uchache ni pamoja na miti ya mitiki, pamoja na ya pine, napenda kusisitiza kwamba pale ambapo Sheria ipo na ilikwishawekwa na Serikali, ni wajibu wetu kufuata masharti ya Sheria hiyo katika kipindi chote ambacho Sheria hiyo bado imesimama.
Mheshimiwa Naibu Spika, iwapo kuna mawazo mengine mapya ambayo ni mazuri, ya kujenga kwa maslahi ya Taifa, basi ni budi kufuata utaratibu wa kawaida wa kisheria kuweza kurekebisha sheria ili kuweza kunufaika na mawazo mapya kama yapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, uvunaji wa mazao ya misitu katika Jimbo la Manyoni Magharibi na Wilaya Manyoni kwa ujumla ulizuiliwa kwa sababu za msingi za uhifadhi. Pale unapoendelea kuvuna unatakiwa uvune ukizingatia sharti la uvunaji endelevu, kama utaendelea kuvuna bila kuzingatia masharti ya uvunaji endelevu, ukakiuka masharti sustainability maana yake ni kwamba utakosa kila kitu kwa sababu misitu hiyo inaweza kupotea kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunapokea maoni yake na kwamba sasa tutakwenda kufanya utafiti wa kisayansi kwenda kuangalia kama zuio hilo sasa limepitwa na wakati, inawezekana msitu huo sasa umeweza kupata hadhi ambayo inawezekana kabisa tukaendelea kuvuna badala ya kusimamisha kama tulivyosimamisha hapo awali. Tutaongozwa na utafiti wa kisayansi ili tuweze kuona kwamba, sasa tunaweza kuendelea kuvuna.
MHE. RISALA S. KABONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza, naitwa Risala Said Kabongo siyo Kabogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuendelea kukauka kwa Mto Ruaha Mkuu mwaka hadi mwaka kunasababisha athari za kimazingira na athari za kukua kwa utalii katika hifadhi hiyo, pamoja na athari kwa wananchi wanaoishi kando kando ya hifadhi hiyo.
Swali la kwanza, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha Mto Ruaha Mkuu ambao ndiyo kiini cha hifadhi ya Ruaha unatiririsha maji yake mwaka mzima?
Swali langu la pili, je, Serikali itawasaidiaje wananchi wanaoishi kandokando ya bwawa la Mtera ambao uchumi wao unategemea uvuvi na kilimo kupitia mto huu wa Ruaha. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimwombe radhi kwa kutamka jina lake ndivyo sivyo, nimepokea masahihisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la mkakati, Serikali inao mkakati siyo kuhusu tu eneo la Bonde la Usangu na Mto Ruaha Mkuu, Serikali inao mradi mkubwa kabisa ambao unakusudia kuboresha shughuli za utalii kwenye eneo la Kusini, mradi ambao unatamkwa kwa kifupi re-grow yaani the Resilient Natural Resources Management for Growth.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mradi huo eneo la Bonde la Usangu ambalo linajumuisha Mto wa Ruaha ni sehemu ya mradi huu. Tunakwenda kuboresha mambo yote yanayohusiana na uhifadhi katika eneo hilo ili kuhakikisha kwamba eneo hilo lote sasa linakuwa na sifa endelevu ya kuwa na kila kitu kilichomo ndani yake katika hali ya uhifadhi unaotambulika Kimataifa na unaokubalika katika kuwezesha shughuli za utalii ziendelee kubaki kuwa bora zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, mradi huu ambao unatekelezwa chini ya Benki ya Dunia sasa hivi upo katika hatua za awali katika siku zijazo za usoni tutautolewa taarifa kuhusiana na jinsi ambavyo tutakuwa tunaendelea kuboresha eneo ambalo nimelitaja.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wananchi wa Mtera inafanana na jibu nililojibu kwa ujumla kwamba mradi huo ninaoutaja ambao upo chini ya Benki ya Dunia unajumuisha mambo yote, yakiwemo kuhifadhi mito iliyomo ndani yake, kuhifadhi misitu iliyopo ndani yake, pia kuangalia maisha ya binadamu na shughuli zao katika eneo linalohusika kama wafugaji, wakulima na wengine wanaofanya shughuli nyingine zote watajumuishwa katika malengo makuu ya mradi huu na kwa hiyo maslahi yao yatazingatiwa Kitaifa katika mradi huo.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza msitu unaozungumzwa haupo, hata athari zinazozungumzwa kwamba vijiji vinavyozunguka watapata athari ya upepo siyo kweli, kwa sababu hata wewe ukisimama mle mita mia tatu unaonekana huo ni msitu?
(a) Je, Serikali kwa sababu inasema ni chujio haioni kwamba sasa ni wakati muafaka wa kulipunguza eneo hilo ikawapa wananchi upande mwingine, na upande mwingine ili wakaendelea na shughuli za kijamii na eneo linalobaki wakaliboresha kwa kupanda wenyewe misitu endelevu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu majibu haya ni ya kudanganywa, je, Naibu Waziri yupo tayari kuambatana nami kwenda kuliona eneo ambalo linasemwa ni hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza, nataka hapa kwa ufupi kabisa tuelewane kwamba, dhana hii ni kwa Watanzania wote kwa nchi nzima. Dhana ya kwamba changamoto za mahitaji ya ardhi kwa ajili ya matumizi mengine ya kibinadamu zitamalizwa kwa kuendelea kumega au kwa kuchukua maeneo yaliyohifadhiwa ni dhana ambayo siyo ya maslahi kwa Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiendelea kufikiria kwamba ardhi iliyohifadhiwa ambayo ipo hivyo ilivyo leo kwa sababu imehifadhiwa kwa muda wote ambao imehifadhiwa, dhana hiyo itatufikisha mahali ambapo uhifadhi huo utapotea na ukipotea athari zake ni pana na kubwa na zinatugusa wote nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli inawezekana ukifika katika msitu huo huoni miti juu, lakini msitu unahifadhiwa kwa ajili ya tafsiri ya misitu ya miti unayoiona ipo juu, lakini pia ni kwa sifa za ardhi pale chini, ndiyo maana tumesema chujio, unaweza usione miti lakini, viumbe vilivyopo pale chini kwenye udongo sifa za ardhi ile iliyopo pale na yenyewe pia ni sehemu ya uhifadhi na ni muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika sehemu ya pili ya swali lake, kwanza siyo kweli kwamba majibu ni ya kudanganywa, lakini hakuna mwisho wa kufanya vizuri, kila unapodhani umefanya vizuri bado kuna kufanya vizuri zaidi. Nipo tayari kuambatana naye kwenda kuboresha uelewa nilionao tayari, kwenda kupata majibu ya pamoja mimi naye wakati tutakapoweza kupanga wote kwa pamoja, ili tuweze kupata hayo majibu sahihi na kuweza kutatua matatizo haya kwa maslahi ya Taifa letu.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Nina swali moja tu la nyongeza, nataka kujua katika hifadhi ya Kitulo iliyokuwepo Makete kuna migogoro mikubwa sana pale kati ya hifadhi ya Kitulo na Vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo. Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha kwamba, matatizo ya mipaka kati ya wanavijiji wanaozunguka hifadhi ya Kitulo na hifadhi ya Kitulo ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Kitulo na migogoro ya ardhi inayotokana na wananchi wanaoishi katika Vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jana wakati tukiwa tunatoa ufafanuzi wa hoja nzima ya migogoro ya ardhi katika maeneo ya hifadhi na yanayopakana nayo, tulitoa ufafanuzi kama ifuatavyo na ambao unahusisha pia hifadhi ya Kitulo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga kwa ajili ya migogoro yote ya ardhi ikiwemo ile inayohusisha hifadhi. Kwa hiyo, kwa hifadhi ya Kitulo tunakwenda kuijumuisha hifadhi ya Kitulo kwenye orodha ya hifadhi zote ambazo zina migogoro kwenda kushughulikia migogoro hiyo kwa kuitazama inahusisha Wizara zipi kati ya zile Wizara sita zilizotajwa. Kwamba, tunakwenda kutazama migogoro hiyo chanzo chake ni nini, inahusu nini na suluhisho lake ni nini kwa kushirikisha Serikali katika Wizara zote zitakazohusika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema jana wakati tunapokwenda kupitia migogoro hiyo tunakwenda kuzingatia maslahi ya Taifa zaidi.
MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2002 mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro ilifanya uhakiki wa mipaka yake na ndipo hapo ilipochukua maeneo ya wananchi katika Vijiji vya Endamaga na Lostete na tangu mwaka huo hadi wa leo kuna migogoro ambayo haiishi ni lini maeneo hayo ya wananchi sasa yatarudishwa kwao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo moja ambalo napenda labda lieleweke vizuri hakuna mahali ambapo Serikali inatwaa ardhi bila kufuata utaratibu. Utaratibu wa Serikali kutwaa ardhi kwa ajili ya maslahi ya Taifa uko wazi, kwa upande wa hifadhi utaratibu huu ni shirikishi na unaanzia kwenye ngazi ya Vijiji vinavyohusika, Halmashauri zinazohusika, vikao vya Mkoa mpaka kufikia vikao vya maamuzi vya Kitaifa ndipo ardhi itatwaliwa kwa ajili ya matumizi kwa maslahi ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo pale ambapo kumetokea sababu yeyote ile ya kutokea kwa mgogoro labda kutoelewana au tafsiri tofauti ya sheria, tafsiri ya GN au matumizi yanayokiuka yale makubaliano ya awali. Hizo ni kasoro ambazo Serikali imekiri na ndiyo maana nimesema awali kwamba tunakwenda kupitia upya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeshajibu swali kama hili hapo nyuma na ninataka kusisitiza tena kwamba, tunakwenda kupitia mgogoro mmoja baada ya mwingine kuangalia ukweli wa mgogoro huo na ufumbuzi wake utapatikana kwa kushirikisha taasisi zote zitakazohusika ndani ya Serikali.
MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, katika ziara yake Mkoani Simiyu Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa maelekezo, kuna mgogoro mkubwa wa hifadhi na wananchi wa Wilaya za Busega, Wilaya ya Bariadi, Wilaya ya Itilima na Wilaya ya Meatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Waziri Mkuu alitoa maelekezo na maagizo kwamba, Mawaziri wanne wakutane mara moja, leo ni miezi mitatu imepita hakuna kinachoendelea.
Je, Mheshimiwa Naibu Waziri lini sasa mtatii agizo la Waziri Mkuu la kukutana na kutatua migogoro hii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali kupitia Waziri Mkuu akiwa Mkoani Simiyu alitoa maelekezo. Maelekezo aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa Simiyu yamekwishaanza kutekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tunayo taarifa iliyoandaliwa ya undani wa orodha ya migogoro yote inayohusika katika vijitabu ambavyo tayari vimeshagawiwa kwa Waheshimiwa Wabunge wote, nia ya Serikali imekwishaelezwa mara kadhaa hapa kwamba umefika wakati sasa baada ya kukusanya taarifa za awali tunakwenda kukusanya Wizara zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kila mmoja anafahamu, Waheshimiwa Wabunge wanafahamu na wananchi wote kwa ujumla wanafahamu kwamba sasa tuna vikao muhimu vya bajeti ambavyo vinakamilika mwisho wa mwezi wa sita, mara tu baada vikao vya bajeti tunakwenda kutekeleza ahadi hiyo ya Serikali ya kwenda kupitia upya migogoro yote hiyo kwa kushirikisha Wizara zote zinazohusika, lakini baada ya kukamilisha jukumu hili lililoko mbele yetu la Bajeti ya Taifa.
MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Wakulima hawa wa Derema 1,128 wamekuwa na malalamiko ya muda mrefu na malalamiko yao hasa yanazingatia kwamba fedha ambazo wamelipwa fidia ni ndogo sana. Fedha hizo zimezingatia shina la mti wa iliki na shina la mti wa karafuu, halikuzingatia mazao ambayo yanatokana na yale mashina.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, kwa kuzingatia ubinadamu, acha mbali hizo sheria: Je, Serikali iko tayari kuwaongezea wakulima hawa wa Derema fidia hiyo?
Pili, ni kweli kabisa kwamba wakulima hawa wanatakiwa kuhamishwa na unapomhamisha mtu inahitaji fedha nyingi sana. Wiki mbili zilizopita Waziri Lukuvi alikuwepo kwenye maeneo hayo ya Kibaranga, ametukabidhi hati ya shamba lililofutwa na Mheshimiwa Rais na tunategemea kuwahamisha watu hawa wa Derema kwenye shamba hilo la Kibaranga, lakini uwezo wa kujenga hawana. Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa tayari kuja kuongea na wananchi hawa wa Derema ili aweze kuwapa matumaini kwamba wataongezewa fidia yao kidogo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kuhusu swali la kwanza; kwanza, nampongeza kwa kuwaonea huruma wananchi wa Jimbo lake, lakini pia nampongeza kwa jitihada anazofanya kwa kuwatetea kila itakavyowezekana ili waweze kupata wanachostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ameshasema hata yeye mwenyewe kwamba majibu haya ni kwa mujibu wa sheria na utekelezaji wa ulipaji wa fidia pale awali ni kwa mujibu wa sheria na sasa anauliza kama Serikali inaweza kuangalia upande mwingine wa ubinadamu, nafikiri hoja ya msingi pale ni kuangalia kwamba fidia ambazo zinalipwa mahali pote, kwa nchi nzima kwa kweli, ziko kwenye viwango ambavyo vinatazamwa kuwa ni vya chini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ubinadamu utatumika katika kwenda kuangalia upya sera na utatumika kwenda kuangalia upya sheria ili tuanzie kwenye ubinadamu lakini turekebishe sera zetu na sheria zetu kwa kuzingatia ubanadamu huo na ukweli na uhalisia ili malipo yaweze kulipwa kwa namna ambayo wananchi watakuwa wameona inakidhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili, nafikiri ni kama mwaliko kwamba niweze kupata nafasi ya kwenda, kwa sababu nikienda nitaona; na kuona ni kuamini. Basi namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, siyo tu mimi kwenda, nafikiri tuongozane naye twende tukaangalie, tuzungumze na wananchi hawa pengine tuwape elimu zaidi na kuweza kushirikiana nao katika kuona ukweli na kuweza kuona jambo gani linawezekana kufanyika kwa maslahi ya Taifa.
MHE. AMINA NASSORO MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa khanga hii ni vazi ambalo mwanamke wa Kitanzania analivaa akiwa nyumbani, ni vazi ambalo analivaa akiwa shambani analima, ni vazi ambalo analivaa anapokuwa kwenye shughuli za kijamii kwenye misiba na kwenye shughuli za harusi, ni vazi ambalo mama anakuwa nalo hata anapokwenda leba. Ni vazi ambalo linampokea mtoto hata anapotoka leba. Ni vazi rasmi la Mwanamke wa Kitanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kanga ambazo zinatengenezwa katika viwanda vyetu vya Tanzania kwa kiwango kikubwa hazikidhi mahitaji ya wanawake wa Tanzania na hasa kwa kuzingatia kwamba vipimo vinavyotumika na ukilinganisha upana na viwango walivyonavyo wanawake wa Tanzania. Wanawake wa Tanzania wanaishi kwa amani na utulivu wako sawa katika afya zao, kanga wanazozivaa haziwatoshi kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna baadhi ya viwanda hata hizi sentimita zilizozungumzwa hawafikii; unakuta urefu ni wa mita 100, sentimita 120 kwa kweli ukiangalia hata wewe mwenyewe haikutoshi hata kwa urefu peke yake. (Kicheko/Makofi)
Sasa swali langu la kwanza, kwa kuwa vazi hili kwa kweli ni vazi la mwanamke wa Kitanzania. Matokeo yake wanawake wameanza kuvaa kanga zinazotoka India na China, wanawake sasa wamehamia kwenye madera, jambo ambalo kwa kweli hawakuzoea, ningependa kujua sasa Serikali inamkakati gani wa kuhakikisha inaielekeza TBS (Shirika la Viwango Tanzania) ili kufuatilia vazi hili, liendane na ubora halisi wa maumbo ya wanawake wa Kitanzania na hasa kwa kuzingatia kwamba kanga hii hata ukiivaa inateleza haifungiki sasa hivi; kwa hiyo hata malighafi wanayoitumia siyo pamba. (Makofi)
Swali la pili, ningependa kujua sasa kwa sababu hili vazi la kanga limekuwa ni dogo, na wanawake wameamua kuachana nalo kwa kuwa na India. Ningependa sasa kujua Serikali ina mkakati gani kwa sababu sasa vazi la dera limekuwa likiwapendeza wakina mama na ni vazi la heshima, ina mkakati gani sasa la kuhamasisha viwanda vya hapa nchini vitengeneze dera badala ya kuwanufaisha mataifa ya mbali? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI (K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Amina Makilagi, Mbunge maalum na machachari kwa akina mama kama ifuatavyo:- (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri kama Serikali ni kweli, kwanza nitambue viwanda tulivyonavyo hapa nchini vingi kabisa tulivirithi toka ukoloni na vichache tulivijenga miaka ya 1970 na vingine miaka ya 1980. Viwanda ambavyo tunavyovitambua kama Mwatex, Murutex, Urafiki, ni vya Nida ndiyo vimeongezeka hivi karibuni. Kwa hiyo ni kweli kabisa viwango vyake ni vya chini na hiyo ninakubali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hatua ambazo Serikali imechukua sasa kwa kutambua mabadiliko ya maendeleo siyo mabadiliko ya uchumi tu hata makuzi ya binadamu. Kwa hiyo ninatambua size za kina mama na hata akina baba, akina baba na nyie mko wapi? Na zenyewe zinakuwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya kwanza ambayo Serikali imechukua viwango vilivyowekwa na TBS vinavyotumika sasa kwa upande wa nguo za kanga kama nilivyosema ni urefu wa sentimita 165 na upana sentimita 116. Lakini kwa upande wa vitenge urefu wa sentimita 200 na upana wa sentimita 116; lakini ni viwango vya mwaka 2009. Kwa hiyo sasa TBS mkakati wa kwanza kabisa inafanyia maboresho viwango hivyo, akina mama sasa mkae tayari kuvaa viwango vikubwa vya nguo. Viwango vinapitiwa na vitaanza kutumika mwezi Juni, mwakani.
Kwa hiyo akina mama Mheshimiwa Mwakilagi nikupongeze sana; Mheshimiwa Naibu Spika hata wewe nadhani unaendelea kukua utavivaa mwaka 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Pili ambao sasa Serikali inafanya, imetenga maeneo maalum kwa ajili ya viwanda vitakavyokuwa vinazalisha sasa nguo aina mbalimbali, vikiwemo vitenge vya kuvaa lakini hata ambavyo vimeshonwa, wametenga hekta 2100 kule TAMCO - Kibaha, pamoja na hekta 431 kule Kigamboni. Kwa hiyo Waheshimiwa akina mama taratibu za kiserikali zinafanyika kuwahakikishia sasa mtavaa nguo bila wasiwasi.
Kuhusiana sasa na madera ni kweli kabisa hata sisi akina baba tunashangaa, unaona akina mama wanavaa madera kila sehemu, kumbe ni kwa sababu hata nguo za kuwabana sasa siyo fashion tena. Sasa hatua za Serikali za makusudi kabisa ambazo imezichukua, sasa hivi vipo viwanda vitatu vinavyozalisha nguo za kuvaa, kiwanda cha kwanza ni cha TUKU ambacho kipo pale Mabibo, lakini viwanda vingine pamoja na Sunflag, pamoja na kile kiwanda cha Mzava karibu na maeneo ya Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mavazi aina ya madera Serikali imekaribisha wawekezaji wa Kichina na Kihindi ili waje wawashonee nguo sasa aina ya madera akina mama mnayoyataka. Kwa hiyo Serikali imeshachukua hatua asante sana Mheshimiwa.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Nina maswali madogo mawili ya nyongeza. Mgogoro huu kati ya wananchi na Hifadhi ya Ziwa Manyara umedumu kwa muda mrefu na chanzo cha mgogoro ni ardhi ya wananchi kuchukuliwa na Hifadhi bila ridhaa yao.
Huko nyuma waliwaruhusu waweze kutumia angalau umbali wa mita 100 kwa ajili ya kuchungia mifugo yao na baadaye hifadhi ikanyang‟anya tena.
Je, Serikali haioni suluhisho la kuondoa mgogoro huu ni kuwaachia hizo mita 100 tu ili mgogoro uishe kabisa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Waziri alipokuja alitoa ahadi kwa wananchi kwamba, kuna fedha shilingi milioni 160 zitapelekwa; shilingi milioni 100 kwa ajili ya madarasa na shilingi milioni 60 kwa ajili ya soko la akinamama, lakini mpaka leo fedha hizo hazijatolewa! Ni lini fedha hizi zitatolewa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kuhusu kuwaachia wananchi eneo linalozungumziwa. Swali la msingi lilikuwa ni nini matokeo ya Kamati. Sehemu yake ya pili, ni lini wananchi watapewa Taarifa ya Kamati hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya kikamilifu ya swali hili yamo katika Taarifa tunayoizungumzia. Kwa hiyo, kwa kuwa, Taarifa tayari ipo na tumemwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba Taarifa hiyo itakuwa tayari kuwasilishwa mbele ya wananchi ndani ya muda wa miezi mitatu. Nikisema ndani ya muda wa miezi mitatu, inaweza kuwa wiki moja, itakuwa ni vema tukasubiri wakati utakapofika tujue wale waliofanya utafiti wa kitaalam na wakaandaa taarifa wamesema nini, kuliko jibu ambalo linaweza kuwa la haraka haraka tu hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi ya fedha halikadhalika kwa sababu waliofanya utafiti wameangalia mgogoro kwa ujumla wake na upana wake na muundo wa Kamati yenyewe iliyofanya uchunguzi ulijumuisha wananchi pia, nina hakika kama hili ni mojawapo ya mambo yaliyozungumziwa, litakuwemo ndani ya ripoti hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo naomba Mheshimiwa Mbunge, akubaliane na mimi tu kwamba kwa kuwa, nimesema ndani ya miezi mitatu na nimesema ndani ya miezi mitatu inaweza kuwa wiki moja, akavumilia tu Wizara itakapokuja kuwasilisha taarifa hii mbele ya wananchi na mambo yote yatakayojitokeza yatakuwa yameamuliwa wakati huo.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Migogoro ya ardhi kati ya hifadhi zetu na wananchi wanaozunguka hifadhi imekuwa ni migogoro ya muda mrefu na imeenea katika nchi nzima. Katika Jimbo langu la Liwale sisi ni miongoni mwa tuliozungukwa na Hifadhi ya Selous.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mgogoro mkubwa sana kati ya hifadhi ya Selous pamoja na Kijiji cha Kikulyungu wakigombea bwawa la Kihurumila. Mgogoro huu umeshapoteza maisha ya watu kwa muda mrefu na hata Mbunge aliyepita wa Jimbo la Liwale mgogoro huu umemfanya asirudi tena Bungeni pale alipotamka Bungeni kwamba anasikia watu wamefariki katika bwawa hilo, badala ya yeye kwenda kujiridhisha na kuangalia hali halisi ya mgogoro huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini basi Mheshimiwa Waziri atashiriki katika kutatua mgogoro huu ili maisha ya watu wa Liwale yasiendelee kupotea wakigombea bwawa la Kihurumila? Naomba majibu.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo amemaliza kuuliza Mheshimiwa Mbunge hivi punde. Waheshimiwa Wabunge karibu wote wanaopakana na hifadhi wakisimama hapa watazungumza matatizo yanayofanana kuhusiana na suala la mipaka baina ya hifadhi na wananchi wanaoishi jirani nazo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niseme tu kwa jibu la ujumla ili kila mmoja ajiandae kupokea matokeo katika hili. Ni kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ambayo inatekeleza Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2015 - 2020, imejipanga vizuri kwa kuweka suala hili baada ya kuliona kuwa ni tatizo kubwa sana; imejipanga vizuri kwa kuliweka waziwazi kwenye Ilani yake na imesema hivi:
“Katika kutatua migogoro hii, Chama kitaendelea kusimamia Serikali yake kuhakikisha kwamba, kinaendelea kujenga mahusiano mema baina ya Hifadhi za Taifa na wananchi wanaoishi karibu na hifadhi hizo kwa namna ambayo wananchi hao watanufaika na uwepo wa hifadhi hizo.”
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, Ilani hiyo hiyo ukurasa wa 23 mpaka 25 inasema:
“Tutasimamia zaidi katika kutatua migogoro ya mipaka kati ya wananchi na maeneo ya jirani na hifadhi kwa kushirikisha wadau katika kuhakiki mipaka ya maeneo ya hifadhi kwa kuweka alama za kudumu, kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi na kuzingatia utawala wa sheria katika kusimamia rasilimali za maliasili.”
Sasa hata wale wanaoingilia katikati ninavyozungumza, pengine wanataka kusema kwamba, hilo ndilo lililoandikwa, lakini wanasubiri utekelezaji. Sasa nataka niseme kwamba, Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga sasa kutekeleza kwa vitendo haya ambayo nimeyasema, kama ambavyo yamekuwa yakisemwa siku zote, lakini sasa hivi tumejipanga vizuri zaidi katika utekelezaji.
MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa migogoro iliyozungumzwa katika hifadhi haitofautiani na malalamiko ya muda mrefu yanayotolewa na Jumuiya za Wapagazi, Waongoza Watalii na Wapishi katika Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro na hifadhi nyingine za Taifa, wakigombana au wakilalamikia Tours Operators wao.
Je, Serikali kwa sababu, inalifahamu hili, ni lini itatatua migogoro hii ili maslahi na mazingira ya kikazi ya Jumuiya hizo za Wapagazi, Waongoza Watalii na Wapishi yaweze kuboreshwa, kama mabalozi wema wa kustawisha utalii katika nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri lenye mwelekeo wa kuboresha zaidi huduma kwenye sekta ya utalii huku tukitambua wote kwamba, utalii unaongoza katika kuliingizia Taifa hili fedha za kigeni. Si zaidi ya wiki mbili nilikuwa KINAPA pale Kilimanjaro National Park, lakini baada ya pale niliungana na Mheshimiwa Waziri, Arusha Mjini ambako tulikutana na Vyama vya Watoa Huduma wote kwenye Sekta ya Utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, zilijitokeza changamoto nyingi, mojawapo ilikuwa ni hiyo na kwamba, sasa Serikali tayari imeshaweka jedwali la changamoto zote hizo ambazo zimezungumziwa na sasa tumejipanga kuhesabu moja baada ya nyingine ili kuweza kupata majawabu na kuweza kutatua migogoro hiyo na matatizo hayo ili tuweze kuboresha Sekta ya Utalii.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Spika ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba kutokana na uhifadhi unaofanywa na wananchi wa Serengeti umesababisha tembo kuongezeka kwa wingi sana.

Mheshimiwa Spika, kwa sensa ambayo imefanyika 2006, kulikua na tembo 3000 na kwa sensa ambayo imefanyika mwaka 2014 tembo wako 7000 na wengi wamehamia maeneo ya West – Serengeti sasa kwa kuwa tembo wameongezeka imekua sasa ni laana kwa wananchi wa Serengeti.

Mheshimiwa Spika, swali, kwa vyote hivi ambavyo Waziri amesema ni ukweli hakuna hata kimoja ambacho kimetekelezwa. Sasa swali kwa Waziri, la kwanza; tungetamani Wanaserengeti kila Kata iwe na game post ambayo game post itakua na gari, itakua na Maaskari na silaha. Je, Wizara iko tayari kujenga game post kwa kila Kata, ziko Kata 10 zinazozunguka hifadhi, mko tayari kutujengea game post na kila game post na askari wake wanalinda mipaka ya Kata husika dhidi ya tembo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nimepitia Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori, Sheria Na. 5 ya Mwaka 2009, kuna kifuta machozi hakuna fidia. Na kifuta machozi kama tembo ameua mtu ni shilingi 1,000,000/= na kama wewe umeua tembo ni 25,000,000/=. Swali, kati ya tembo na mtu nani wa thamani?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, Serikali katika hatua ya kwanza kabisa inampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia jitihada za Serikali katika uhifadhi. Takwimu za ongezeko la tembo ni faraja kwa Taifa hili kwa sababu kila mmoja wetu anafahamu faida za uwepo wa wanyamapori na faida za uhifadhi katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la hatua zilizochukuliwa napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ni wiki mbili tu zilizopita nilikuwa Serengeti na haya niliyoyasema hapa sikuyaandika tu kutoka kwenye karatasi isipokuwa nimeshuhudia yakiwa yametekelezwa katika hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu swali lake la uanzishwaji wa game posts katika kila Kata hili ni wazo jema, unapotaka kuanzisha jambo ambalo ni jipya ni lazima kujipa fursa kwanza ya kufanya utafiti uliokamilika uweze kujiridhisha juu ya umuhimu na uwezekano na ukaangalia kila aina ya jambo ambalo ni la umuhimu kabla ya kutekeleza mpango wowote unaoufikiria.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunalipokea, tutalifanyia kazi na itakapoonekana kwamba ni jambo ambalo ni vema tukalitekeleza basi Serikali italitekeleza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kifuta machozi kuwa kidogo, katika jibu langu la msingi nimeeleza pale mwishoni kwamba Serikali inatambua juu ya changamoto ya kwamba kifuta jasho au kifuta machozi vyote kwa pamoja hivi kila kila kimoja havitoshi, yeye ameangalia tu upande wa maisha lakini pia hata kwenye mali, mali zinazoharibiwa wakati mwingine ukiweka ulinganifu wa kiasi cha mali kilichopotea na kiwango kile kinacholipwa mara nyingi kinakuwa ni kidogo.

Mheshimiwa Spika, lakini nimesema kwenye jibu la msingi kwamba Serikali inachukua hatua ya kupitia viwango hivyo na upitiaji wa Kanuni utakapoonekana kwamba, iko haja ya kuweza kufanya mabadiliko basi tunaweza kufanya mabidiliko hayo kwa mujibu wa sheria.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kutoa majibu ya nyongeza baada ya majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Spika, ningependa sana niwapongeze wananchi wa Serengeti kwa moyo wao na juhudi zao katika kuhifadhi wanyamapori, ninaamini kabisa kama wananchi wa Serengeti wangekuwa hawahifadhi wanyama wale walioko pale ingekuwa vigumu sana kwa pori lile kuwa zuri na pori ambalo lina kiwango cha pili kwa ubora dunia nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu ambao wanaua tembo ni majangili siyo wananchi wa Serengeti na ndiyo maana watu ambao wanawaua wale tembo kama wanaua kwa makusudi kama ambavyo inatokea mara kwa mara ndiyo maana wanachajiwa fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, lakini malipo haya hayalinganishi binadamu na wanyama. Lengo ni kuhakikisha kwamba watu wenye nia mbaya hawauwi wanyama bila sababu, lakini pia ni kuhakikisha kwamba Serikali inashirikiana na wananchi katika kuomboleza matukio ambayo yanaweza kutokea kwa wanyama kuwaua wananchi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika kwa baadhi ya majibu ya uongo ambao Mheshimiwa Naibu Waziri ameyajibu. Mimi ndio
Mbunge wa Jimbo husika na kuna mwananchi wangu nimemhudumia katika Hospitali ya DDH. Aliyekupa hizo taarifa kamwulize vizuri, amekuongopea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naenda sasa kwenye swali. Sheria ya Kazi Na. 6, mtu anapokufa kazini, analipwa fidia shilingi milioni 10. Hawa wananchi wangu walikuwa kazini, mbali na kwamba wamejiajiri wenyewe, mwalipe fidia, siyo kifutajasho cha laki moja moja. (Makofi)
Swali la pili; Mheshimiwa Waziri, tatizo la mamba katika vijiji nilivyokwambia ni kubwa sana, hata kwa kaka yangu kule Mheshimiwa Kangi, wananchi wanavua kienyeji kwa kutumia kuku. Lini Wizara yako itapeleka wataalam mwavue? Wananchi wangu wanakufa kila siku wanakuwa vilema halafu unatoa majibu mepesi hapa!
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba umesema swali la kwanza pengine lingejibiwa na Waziri wa Sheria lakini napenda kutoa sehemu ya majibu.
Mhehimiwa Naibu Spika, Serikali inafanya kazi zake kwa kutumia mfumo wake. Kwa hiyo, taarifa ambazo zimo katika majibu niliyoyatoa zimetoka kwenye Halmashauri ya Bunda na vyombo vya Serikali vilivyopo kule. Kwa hiyo, kwa kuwa Mheshimiwa Ester Bulaya ni Mjumbe wa Halmashauri ya Bunda, anaweza kwenda kuwahoji waliotoa taarifa hizi ambao ni Halmashauri inayohusika kwamba kwa nini wameleta majibu ya uongo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu fidia kwamba Serikali inalipa kifuta jasho au kifuta machozi na siyo fidia; na Mheshimiwa Mbunge angependa badala yake tulipe fidia, kwa sababu kiwango cha shilingi laki moja ni kidogo; nchi hii inaendeshwa kwa mujibu wa sheria. Hakuna namna yoyote ambayo unaweza kuendesha nchi bila kufuata sheria, kanuni na taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ulipaji wa kifuta jasho na kifuta machozi ni utaratibu uliopitishwa kwa mujibu wa sheria ambayo imepitishwa na Bunge hili. Iwapo itaonekana kwamba utaratibu huo haufai kwa namna yoyote ile, ni wajibu wa Waheshimiwa Wabunge kwa niaba ya wananchi, Mheshimiwa Ester Bulaya akiwa mmoja wao kuleta mapendekezo ya kufanya mapitio upya ya Sheria hii na kama itafaa, pengine Serikali inaweza ikaanzisha utaratibu mwingine badala ya huu.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuongezea jibu zuri ambalo limetolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwanza napenda niseme kwamba Wizara itafuatilia kuona kama kuna taarifa zaidi ya zile ambazo tunazo ili tuweze kuzishughulikia kama ambavyo tumeshughulikia sheria hizo nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, mimi sio Mwanasheria, lakini najua kwa sababu nilifanya kazi kwenye Wizara ya Kazi, kwamba hakuna Sheria ya Kazi ambayo inafidia raia wakati yuko kwenye shughuli zake. Sheria ile ya Kazi ni ya wafanyakazi kama ambavyo inajulikana kwenye sheria ile.
MHE. HASSAN S. KAUNJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwanza kwa majibu ya ziada ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Swali langu la msingi ilikuwa ni lini, kwa maana ni mwaka gani katika miaka hii mitano au bajeti ipi hizi program za Maendeleo ya Sekta ya Utalii Kusini zitaanza?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kwa maana ya vivutio alivyovitaja, sambamba na vivutio vingine vya fukwe za Kisuele na Mitema ambazo ni bora kuliko zote katika ukanda wa Pwani ya Afrika Mashariki, kuanzia Somalia mpaka South Africa: Je, yuko tayari kuviwekea vipaumbele katika kuvitangaza kupitia taasisi zake zinazotangaza utalii wa nchi hii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Kaunje, kwa namna ambavyo ameanza kwa kasi kubwa kuweza kutetea eneo la Kusini ili utalii sasa uweze kuelekea upande wa ukanda huo, kwa maana ya Southern Circuit badala ya hali ambayo iko hivi sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la lini; nimezungumzia Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano kwenye jibu langu la msingi, lakini pia nimetaja mradi wa Regrow ambao nilisema na wenyewe ni mradi ambao unakwenda kuboresha utalii katika ukanda wa kusini. Sasa kuhusu lini, nataka kusema, kuhusu mradi wa Regrow tayari mradi huo umeshaanza na uko katika hatua za awali na miradi mingine ambayo itakuwa inaunga mkono jitihada za utalii kusini itaweza kupangwa katika bajeti zijazo, wakati kwa sasa hivi tunatekeleza mradi huu wa Regrow ambao wenyewe tunautekeleza kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu fukwe za Mitema na nyinginezo kuweza kupewa kipaumbele, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, kwamba Mikoa ya Lindi na Mtwara ina utajiri mkubwa sana wa fukwe za bahari, tofauti na maeneo mengine ambako kuna fukwe za Maziwa; Lindi na Mtwara kuna utajiri mkubwa sana wa fukwe za bahari.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka mitano, ambao unaanza na mpango huu wa mwaka wa kwanza wa 2016/2017, hatua ya kwanza tunayokwenda kuifanya ni kutembelea maeneo hayo yote na kuweka matangazo ya kutosha ili kuweza kuwavutia wawekezaji mbalimbali kuweza kuboresha miundombinu katika maeneo hayo ili fukwe hizo ziweze sasa kushiriki katika Sekta ya Utalii kwa tija zaidi.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni muda ni muda mrefu sana mgogoro wa Kagera Nkanda umekuwa ukiongelewa humu Bungeni lakini maka sasa hakuna ufumbuzi ambao umeshapatikana. Na kwa kuwa watu wanaongezeka lakini ardhi haiongezeki, ni lini Serikali italeta sheria Bungeni ili ifanyiwe marekebisho kusudi mipaka iweze kusogezwa wananchi wapate maeneo ya kulima?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe taarifa tu kwamba ni kweli migogoro inayohusisha mipaka kwenye hifadhi iwe hifadhi za misitu na hifadhi za wanyamapori ni mikubwa na ni kweli sasa imekuwepo kwa muda mrefu. Lakini napenda tu nitoe taarifa kwamba kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi sasa tunakwenda kupata ufumbuzi wa matatizo haya, tutapiga hatua na kuweza kuyapunguza matatizo haya kama sio kuyamaliza baada ya zoezi tunalolitaja ambalo litashirikisha Wizara sita kwenda kuangalia hasa uhalisia wa matatizo kwenye mipaka hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema awali na isichukuliwe kwamba utatuzi au ufumbuzi wa changamoto za ardhi iko kwenye hifadhi za taifa peke yake, hapana, ndiyo maana tunasema sasa tunakwenda kwa ujumla wetu Wizara sita zote ambazo ni watumiaji wa ardhi ili tuweze kwenda kubaini kwamba ni kweli kuna uhaba wa ardhi au kuna matatizo mengine yanayosababisha watu kuingia kwenye hifadhi? Kwa hiyo, tutakwenda kuchakata na kuangalia mahitaji yapi ya ardhi yanahitaji ardhi ambayo tunaweza kuipata wapi kabla hatujaingia kwenye hifadhi ambako kumezuiliwa kwa mujibu wa sheria.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona.
Kwa kuwa tatizo lililopo Kagera ni sawasawa na tatizo lililopo kwenye Jimbo la Geita Vijijini katika Msitu wa Lwande. Sisi kama Halmashauri tulipendekeza hekta 7,000 zirudishwe kwa wananchi kutoka kwenye hekta 15,000; na tukapeleka maombi yetu Wizarani. Je, ni lini Serikali itajibu maombi ya Wilaya yetu kuhusiana na hizo hekta 7000?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nimetoa maelezo ya awali ambayo napenda niyasisitize tena; hakuna jambo zuri katika kushughulikia changamoto yoyote ile kama kufanya utafiti, kama kwenda kutafuta kiini cha tatizo, usipofanya hivyo ukatafuta suluhisho utafuta suluhisho pengine ukapata suluhisho la muda tu. Lakini ukitaka suluhisho la kudumu lazima ufanye utafiti, kama vile ambavyo ukiwa na maradhi unataka kutibiwa unakwenda kwanza maabara unafanya vipimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumesema tunataka kwenda kwenye maeneo haya yote kwa ujumla wake ikiwemo kwenye eneo ambalo Mheshimiwa Joseph Musukuma analizungumzia. Napenda nimuombe Mheshimiwa Musukuma avute subira kidogo; maombi aliyopeleka Wizara ya Maliasili na Utalii hayatashugulikiwa na Maliasili tu peke yake. Tumesema tunakwenda kushirikisha Wizara zote ambazo ni wasimamizi au ni watumiaji wa ardhi ikiwemo TAMISEMI ambayo wamesema kwamba wamepitisha maombi kule, tunakwenda kushirikiana nao kwenda kutafuta ufumbuzi ambao utauwa ufumbuzi wa kudumu.
MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Mgogoro uliopo Kasulu - Kagera Nkanda unafanana kabisa na mgogoro ambao upo Wilaya ya Kakonko ambako tunayo mbuga ya wanayama ya Moyowosi na Kigosi inayozungumzwa. Vijiji vya Mganza, Itumbiko, Kabingo na Kanyonza vinapakana na maeneo hayo na; kwa hiyo vimekosa ardhi kabisa ya kutumia kwasababu ya ongezeko la watu. Kwa hiyo, nauliza swali; ni lini mchakato huo wa Wizara ya Maliasili na Utalii itaiona hoja ya wananchi kuongezewa ardhi kutoka kwenye hifadhi badala ya hifadhi kuwa na ardhi kubwa kuliko wananchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi maswali yote yanayohusiana na migogoro ya mipaka ambayo unaweza ukaiita migogoro ya ardhi, lakini inayohusiana na hifadhi yanakuwa yanahusiana na maliasili na utalii. Ukizungumzia migogoro ya ardhi hiyo hoja ni pana zaidi kuliko hivi sasa.
Kwa hiyo, suala ni lini tutashugulikia mgogoro wa Kakonko kule jibu ni lile lile, kwamba tuvute subira tusubiri twende tufike kwenye maeneo haya tufanye utafiti, tufanye ukaguzi ili twende tukafanye team work.
Mheshimiwa Naibu Spika, bila kwenda kukagua kwa pamoja tukaangalia pengine tunaweza tukakurupuka na majawabu ambayo si sahihi. Ipeni nafasi Serikali tufike kule, Wizara zote sita kwa ujumla wetu tukishirikisha TAMISEMI lakini pia tukishirikisha hata wananchi wenyewe ambao ndio wanaguswa na matatizo na changamoto hizi. Zoezi zima litakuwa ni shirikishi, kwa hiyo tutapata majawabu ambayo yatakuwa ni ya kudumu.
MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa mgogoro uliopo katika Pori la Kagera Nkanda unataka kufanana na matatizo yaliyopo katika Pori la Burigi na Kimisi hususan maeneo yaliyopo katika Jimbo la Ngara; kama ambavyo tangu mkutano wa pili wa Bunge niliweza kueleza na hata katika mchango wangu wa bajeti ya maliasili; kwamba tangu mwaka 1959 mrahaba ule wa asilimia 25 ambao unatakiwa kurudishwa kwenye Halmashauri kutokana na vitalu vya uwindaji haijawahi kupelekwa kwenye Jimbo la Ngara.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, Waziri wa Maliasili na Utalii anaweza kuwaeleza wananchi wa Jimbo la Ngara na Halmashauri ya Wilaya ya Ngara, ni lini pesa hizo zitapelekwa, ambazo tangu mwaka 1959 mpaka leo hazijapelekwa?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la mrabaha likilinganishwa na swali la msingi ambalo nimelijibu ni mahususi kidogo na bila shaka linahitaji takwimu na linahitaji taarifa ambayo ni mahususi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimuahidi Mheshimiwa Mbunge baada ya kipindi hiki cha asubuhi, mchana awasiliane na mimi nitaweza kumpa jibu sahihi kwa swali lake ambalo ni mahususi.
MHE. DKT. SHUKURU KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu ingawa ni majibu ambayo mimi na wananchi wangu wa Bagamoyo yanatupa matatizo. Sasa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kama atakubali kuielekeza timu hii ya pamoja iliyoundwa ili iweze kukutana na wawakilishi wa wananchi hawa akiwemo Mbunge na Waheshimiwa Madiwani wa jimbo la Bagamoyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, TANAPA inawatoza fedha wananchi wa Makurunge na Matipwili wanapovuka daraja eneo la Gama katika Mto wa Wami wanapokuwa wanafanya shughuli zao, mtu Shilingi 5,000 na gari Shilingi 25,000, je, nini kauli ya Serikali kuhusu uhalali wa tozo hiyo?
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dokta Shukuru Kawambwa Mbunge wa Bagamoyo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ushauri alioutoa nitaufikisha mbele ya Kamati hii maalum. Kwamba pamoja na utaratibu waliojiwekea wa kuweza kutimiza malengo yao kwa mujibu wa kazi walizopewa na hadidu za rejea.Ni jambo jema na ni wazo zuri na litaweza kuboresha matokeo ya kazi wanayoifanya kwa kuwashirikisha pia Mheshimiwa Mbunge pamoja ma Madiwani wanaohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili linlohusiana na TANAPA kuwatoza wananchi ada hizi; kwanza nalisikia kwa mara ya kwanza na kwa kuwa ni suala jipya kujua mantiki yake na sababu zake kwanini liko hivyo nahitaji muda kidogo, lakini kwa wakati huu nikiwa nimesimama hapa naliona lina ukakasi wa namna Fulani. Kwa hiyo namuomba Mheshimiwa Mbunge anipe nafasi, nalishughulikia mara moja katika kipindi hiki hiki cha Bunge na pengine kwasababu ya uzito wake kuwa mkubwa, mchana huu nikutane naye, nitakuwa nimeshafanya mawasiliano angalau ya awali kujua likoje halafu tuweze kutafuta suluhisho lake.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Pamoja na majibu haya ambayo ameyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mazingira ya kimondo chenyewe yako kwenye hali mbaya sana, na ukiangalia miundombinu na barabara zinazoenda kule ziko kwenye hali mbaya sana, hivi sasa hivi kimondo kile hata uzio wa kukizunguka kimondo kile ku-protect haupo. Sasa je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha mazingira ya kimondo kile ili kiwe ni kivutio kizuri sana kwa utalii pamoja na kuinua pato la Mkoa mpya wa Songwe na Jimbo langu la Vwawa?
Mheshimiwa MWenyekiti, swali la pili; kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ilishaandika barua ya kuomba Wizara hii ikikabidhi kimondo kwenye Halmashauri ili waweze kukiendeleza na kuweka vivutio mbalimbali ikiwa ni pamoja na migahawa, hoteli na vitu mbali mbali vitakavyowavutia watalii wa ndani na nje, Serikali ni lini sasa itakubali kukikabidhi kimondo hicho katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi?
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza linahusu changamoto ya miundombinu kutokuwa bora au kutokuwa rafiki kwa shughuli za utalii kwenye eneo hili ambako kimondo chetu kipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua wazi kwamba ili kuweza kuboresha utalii miongoni mwa maeneo ambayo yanatakiwa kutiliwa mkazo, na kwakweli yanatiliwa mkazo na Serikali, ni pamoja na kuboresha miundombinu kwenye maeneo yenye vivutio kama hili la kwenye kimondo cha pale Mbozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya Serikali ambayo ametaka kuifahamu Mheshimiwa Mbunge ni kuboresha miundombinu hiyo kwa kutumia bajeti zake lakini pia kwa kushirikisha wadau. Kwa hiyo wakati Serikali inaendelea na utaratibu wa kutumia fedha zake za bajeti kuboresha miundombinu bado mheshimiwa Mbunge kwa kuungana na Serikali aweze kutafuta namna ambayo anaweza kushirikiana na Serikali kuweza kuwafikiwa wadau mbalimbali kwenye eno la Mbozi ikiwa wanaweza kufanya jitihada kuungana na Serikali katika kuboresha miundombinu kama alivyoitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kimondo kukabidhiwa kwa Halmashauri, suala hili haina tofauti kubwa sana kiuendeshaji, Serikali ni ile ile, Halmashauri bado ni Serikali na Serikali kuu bado ni Serikali. Mawazo mema na mazuri yanaweza kupokelewa kulingana na ubora wake na wakati. Kwa hiyo nimshauri mheshimiwa Mbunge ashirikiane na Halmashauri na washauri waweze kutuandikia Wizarani tutaweza kupima kuona ikiwa sababu hizo za kukabidhi kimondo hicho kwa Halmashauri linaweza likafanya eneo hilo likafanyika utalii kwa namna bora zaid na kwa tija zaidi kuliko ilivyo sasa.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Serikali inawauzia kiwanda cha Mgololo nusu ya bei 14,000 badala ya 28,000; je, Wizara iko tayari sasa kuwauzia pia wavunaji wadogo wadogo wa Mafinga na Wilaya ya Mufindi kwa ujumla nusu ya bei kama inavyouzia MPM?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa kumekuwa na ujanja ujanja mwingi katika suala zima la utoaji vibali na kama nilivyosema jana tuko karibu na waridi lazima tunukie waridi; je, Wizara iko tayari sasa katika kutoa vibali, itoe by name and by location ili kusudi wakazi wanaozunguka msitu waweze pia na wenyewe kunufaika kwa kupata vibali hivyo badala ilivyo sasa orodha inaonesha kuna watu wanapata vibali lakini majina ya watu hao sio wanaozunguka msitu. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza kuhusu nusu bei kwa kiwanda cha Mgololo na uwezekano wa kuuza kwa bei hiyo hiyo bidhaa hiyo kwa wafanyabiashara wadogo wadogo au mwananchi mmoja mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili hoja yake ni miongoni mwa hoja kubwa, nzito zilizotolewa wakati wa mjadala wa bajeti jana na kwa sababu hiyo maandalizi ya majibu ya kina yapo kwenye majawabu ya ufafanuzi wakati Mheshimiwa Waziri atakaposimama na nitakaposimama mimi. Sasa kwa kuokoa muda namwomba Mheshimiwa Mbunge asubiri wakati tutakapokuwa tunahitimisha hotuba jioni. Atapata majibu ya kina kuhusu swali hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili la ujanja ujanja na uwezekano wa kutoa vibali kwa majina na kwa maeneo; jawabu ni kwamba jambo la msingi hapa linalohitajika ni uwazi. Wananchi wangependa kuona uwazi zaidi kuliko ilivyo sasa kwamba tutakapotoa takwimu kwamba watu gani wamepata mgao, basi ni vyema watu hao wakaonekana miongoni mwa jamii wazi wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nimetembelea kwenye shamba la msitu la Sao Hill moja ya mambo ambayo nilisema ni kwamba, kuanzia baada ya ziara yangu wakati utakapofika licha ya ule utaratibu wa kusubiri kupitia mwongozo mzima, hili moja ni la wazi kabisa kwamba tunakwenda kushirikisha Serikali tangu kwenye ngazi ya vitongoji na vijiji si tu kwamba kumtaja mtu mmoja mmoja lakini Serikali kwa ujumla wake kwa kutumia mfumo wake utashirikishwa katika zoezi zima la ugawaji wa malighafi hizi.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mpaka wa Tanzania katika eneo la Rusumo mpaka unapoenda Kagera ni hifadhi, lakini mpaka huo kwa upande wa Rwanda ni vijiji ambavyo viko mpaka kwenye Mto Kagera, kwa sababu Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwamba changamoto zilizopo katika hifadhi hiyo ni pamoja na hifadhi hiyo kutumiwa na wahamiaji haramu, watu wanaopitisha silaha na ujambazi.
Je, ni lini Mheshimiwa Naibu Waziri atahakikisha kwamba eneo hilo linalindwa kwa usalama wa nchi? Hilo swali la kwanza.
Swali langu la pili, katika hifadhi hizo za Burigi na Kimisi kuna Maziwa Ngoma na Maziwa Burigi, ambayo miaka yote yamekuwa yakitumiwa na watu kutoka nchi za jirani kwa uvuvi katika maziwa hayo na kwa ulinzi mkubwa wa askari wa wanyamapori. Ni lini Serikali itaanzisha seasonal fishing kwa Watanzania ili waende kuvuna maliasili hiyo?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la kwanza lini Serikali itaimarisha ulinzi kwenye maeneo hayo, nimejibu kwenye swali la msingi, kwamba mpaka sasa hvi tunavyozungumza, changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza katika eneo tunalolizungumzia zimekuwa zikishughulikiwa kwa pamoja kwa ushirikiano baina ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Kamati ya Ulinzi ya Wilaya, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ameeleza kwamba yapo mashaka ambayo yanaendelea kuongezeka kila siku, basi Wizara yangu itaendelea kushirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya na Mkoa kuweza kuona namna gani tunaweza kuboresha vizuri zaidi au kufuatilia zaidi ambazo zinaonekana kujitokeza upya kwa sasa hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala ni lini, napenda pia nimkumbushe Mheshimiwa Kanyasu kwamba tumesema mara tu baada ya Bunge hili tunapita maeneo yote ambayo yana changamoto za kiulinzi na usalama kuhusiana na masuala ya mipaka ili tuweze kuboresha vizuri zaidi changamoto za ulinzi na usalama na changamoto za migogoro ya ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la mabwawa yaliyopo ambayo yana samaki na kwamba kwa sababu yapo ndani ya hifadhi basi kwa mujibu wa sheria wananchi hawaruhusiwi kufanya uvuvi. Napenda kujibu kwamba sababu za kuzuia kufanya uvuvi zitakuwa ni sababu za kiuhifadhi, lakini kwa kuwa kuhifadhi maana yake siyo kuacha kutumia maana yake ni kutumia kwa busara na hekima, kuhifadhi maana yake ni kutumia ukijua kwamba ipo kesho na kwamba unaweza ukatumia leo ukijua kabisa kwamba kesho utahitaji kutumia kitu kile unachokitumia leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo kwa maana ile ya kufanya uhifadhi endelevu tutaliangalia suala hili kuona ni namna gani tunaweza tuka-engage wananchi waliopo katika maeneo haya waweze kufanya uvuvi kama taratibu za kisayansi za uhifadhi zitaruhusu. Lakini tunakwenda kufanya jambo hili kwa pamoja liwe shirikishi ili wote tuone ukweli sasa kwamba kitakachofanyika kiwe kwa maslahi ya Taifa.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu ambayo hayatoshelezi.
Kwa kuwa mimi nimezaliwa na kukulia katika mbuga hii, ni mashahidi kwamba mbuga hii ilitelekezwa, kwa hiyo, wananchi wengi wakulima na wafugaji walihamia katika mbuga hii. Matokeo yake wanyama na hao ndege anaosema wametoweka; kama wamebaki ni sehemu ndogo sana; na kwa kuwa eneo hili mwaka 2014 lilisababisha mauji ya wakulima watano kutokana na mgogoro wa wakulima: kwa nini Serikali isikubali ombi hili? Swali la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa sasa hivi nchi inakabiliwa na migogoro ya wafugaji na wakulima, sisi sote ni mashahidi; na kwa kuwa mwaka 2011 Serikali hii ilifanya tathmini ya mbuga zile ambazo zimepoteza sifa na Wembere ilikuwa ni mojawapo; kwa nini Serikali isilitazame upya jambo hili na kuitenga mbuga hii ili wananchi wanaoishi kwenye eneo hilo waweze kulima na kufuga bila kugombana; lakini pia wanaweza kubakiza eneo dogo kwa ajili ya hawa ndege hawa anaowasema? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili la Wembere hivi sasa ninavyozungumza, limegawanywa katika vitalu vinne; Kitalu kinachoitwa Wembere Open Area Central One, kitalu kinachoitwa Wembere Central Area Two, Wembere Game Controlled Area upande wa Kusini, lakini pia upande wa Kaskazini kuna Wembere Open Area, vyote hivi vikiwa ni vitalu vinavyopaswa kuendesha shughuli za uwindaji wa kitalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, mojawapo ya kitalu, kwa mfano, hiki cha upande wa Kaskazini, Wembere Open Area hakijawahi hata kupata mwekezaji kwenye shughuli hizo za uwindaji. Lakini vipo vitalu ambavyo vinafanyakazi, kwa mfano kile cha Open Area Central One, kinatumika na ndiyo hicho ambacho nimesema ni mojawapo ya vitalu vinavyoiingizia fedha Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tunazungumzia mazingira halisi ambayo Mheshimiwa Mbunge anatoka, wakati huo huo tunachokizungumzia ni suala la utaalam vilevile, basi nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba arejee azma ya Serikali tuliyoitangaza hapo awali, kwamba sasa tunataka kufanya zoezi Shirikishi; yeye pamoja na wananchi kwenye eneo linalohusika kwenye maeneo hayo ya Wembere pamoja na timu ya wataalam ambayo tayari tumeshasema baada ya Bunge hili tunakwenda kwenye maeneo hayo kuhakiki, twende tukaoneshane.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuchanganye utaalam na maoni ya wananchi ili tuweze kufikia muafaka sasa kujua kama kuna eneo ambalo ni sehemu ya eneo hili ambalo litaonekana halifai kuendelezwa tena kwa shughuli hii ambayo sasa hivi inaendeshwa kwa mujibu wa sheria, basi itakuwa hivyo. Kwa sasa hivi tutaendana na sheria kama ilivyo mpaka hapo mabadiliko yatakapofanyika baada ya zoezi lile la Serikali.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuulizwa swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo yaliyoko katika swali namba 279 yanafanana sana na hali halisi iliyoko Urambo katika Kata ya Nsenda ambako wakulima wa Lunyeta na Kangeme walichomewa mahindi yao kutokana na mgogoro wa mipaka kama ulivyoelezwa katika suala hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mgogoro huu umewaacha wakulima bila kujua hatima yao na kusababisha usumbufu sana wa kupata chakula; na Serikali ilikiri kwamba ilifanya makosa kuwachomea wakulima ambao walikuwa wamelima katika eneo hilo, je, Serikali iko tayari sasa kufuatana na mimi kwenda kuangalia hali halisi ili kutafuta ufumbuzi wa kudumu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tunazo sheria, lakini ni kweli pia kwamba kuwa na sheria ni sehemu moja au ni jambo moja, lakini utekelezaji wa sheria ni jambo lingine. Inawezekana kabisa kwamba mahali pengine utekelezaji wa sheria unaweza kuwa ni utekelezaji wa sheria unaovunja sheria. Sasa pale ambapo tayari kuna sheria na sheria zinatakiwa kusimamiwa, Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria, lakini tunatoa wito kwanza kwa watu wote ambao wanatekeleza sheria, hasa zile sheria ambazo ziko chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, waweze kutekeleza sheria hizo bila kukiuka sheria zenyewe, lakini bila kufanya mambo ambayo yanakwenda kinyume cha kanuni na taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala mahsusi ambalo Mheshimiwa Mbunge ameliuliza, linalohisiana na eneo alilolitaja, napenda kumuahidi kwamba nikitoka hapa nitakwenda kulifuatilia zaidi na mimi nilifahamu kwa sababu ni mahsusi ili niweze kuona kama tunaweza kupata suluhisho katika kipindi hiki ambacho tuko Bungeni; lakini kama itabidi kwenda kuangalia, basi mara tu baada ya kumaliza Bunge la Bajeti, nitaweza kuandamana naye kwenda kuona kuna nini ili tuweze kupata ufumbuzi.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Migogoro ya ardhi ambayo inajitokeza kati ya hifadhi na wananchi nayo yanajitokeza katika Pori Tengefu la Bonde la Kilombero. Tumeiomba Serikali, naomba niwaulize hapa Serikali, ni lini sasa mtarudisha ardhi ile ya Buffer Zone katika Pori Tengefu la Kilombero?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza niseme kwamba Buffer Zone tafsiri yake ya moja kwa moja isiyohitaji utaalam mwingi sana ni eneo ambalo linapaswa kuwa siyo la yeyote kati ya pande mbili zinazopakana. Eneo hilo kwa mujibu wa kanuni na taratibu, linapaswa kuwa ni eneo ambalo shughuli za uhifadhi zinakuwa mild, lakini pia shughuli za matumizi ya kibinadamu na zenyewe zinakuwa mild kwa maana ya kwamba siyo eneo ambalo linatumika moja kwa moja kwa asilimia mia moja na pande zote mbili zinazopakana. Kwa hiyo, kusema kwamba lirudishwe kwa wananchi, pengine inaweza kuwa siyo sahihi sana kwa sababu halijawahi kuwa kwa asilimia mia moja upande wa hifadhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotangulia kusema na ninarudia tena, mazoezi haya yote ya kupitia hifadhi baada ya hifadhi; iwe hifadhi ya misitu, iwe hifadhi ya wanyamapori au hifadhi nyingine yoyote ile chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii; maeneo yote hayo yameorodheshwa kama sehemu ya migogoro ya ardhi na yameorodheshwa hivyo na Wizara ya Ardhi. Pia tunakwenda kufanya team work miongoni mwa Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ardhi yenyewe, TAMISEMI, eneo ambalo sasa Mheshimiwa Mbunge atashirikiana na Serikali ya Wilaya pale, lakini pia Wizara ya Nishati na Madini, pale patakapokuwa panahusika na mambo ya madini; lakini pia masuala ya maji kwa sababu tunahusika pia. Kwa kutunza misitu tunatunza pia vyanzo vya maji, basi pale itakapobidi kwamba kuna chanzo cha maji tunataka kukifanya kiwe endelevu, kukilinda, basi na Wizara ya Maji itahusika. Kwa kuanzia ni Wizara hizo tano.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba wananchi wote na kupitia swali hili la Mheshimiwa Mbunge, wawe wavumilivu katika kipindi hiki ambacho ni kipindi cha mpito ambapo Serikali sasa inakwenda kutafuta majibu ya kudumu kwenye migogoro hii ya mipaka na hifadhi na migogoro ya ardhi kwa ujumla.
MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali iliongeza mipaka yake ikawafuata wananchi katika vijiji vinane vya Mwamumtani, Mwalali, Ndung‟wa, Ndinho, Ntantulu, Kiliju, Longalombogo na Shishani na haikuwashirikisha wananchi, je, ni lini sasa eneo hili litarudi kwa wananchi kwa kuwashirikisha wananchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa amesema umegaji wa eneo hili haujaleta tija na haujamaliza changamoto ya wananchi na kwa kuwa Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni akiwa kwenye Kijiji cha Nanga katika Kata ya Kinameli aliliona hili na alitaja Sheria ya Ardhi, Na.4 akasema kwamba akiwa Rais eneo hili atalirudisha kwa wananchi. Je, kwa nini Mheshimiwa Naibu Waziri anapingana na ahadi ya Rais?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nazingatia kujibu kwa kifupi, moja kwamba zoezi lililofanyika huko nyuma la upanuzi wa mipaka halikushirikisha wananchi na ni lini Serikali itashirikisha wananchi? Kwanza si kweli kwamba Serikali inaweza kupanua mipaka ya eneo lolote lile hasa mipaka ya wananchi wanaopakana na hifadhi bila kushirikisha wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, bado Serikali ina nia njema ya kufanya zoezi la kupitia mipaka kwa namna bora zaidi kuliko ilivyokuwa siku za nyuma. Ndiyo maana nimesema kwenye jibu la msingi kwamba tunakwenda sasa kushirikisha Wizara nyingi zaidi na tunakwenda kufanya ushirikishwaji zaidi katika hatua hii lakini mara hii tunakwenda kuweka vizuri kumbukumbu ili hata vizazi vijavyo vije kuona kwamba zoezi hilo lilifanyikaje kuliko ilivyokuwa siku za nyuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la ahadi ya Mheshimiwa Rais ikihusisha Sheria Namba 4, napenda kujibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza haiwezekani kabisa tukafika mahali tukaweza kupingana na maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Hilo ni jambo ambalo haliwezekani kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama alikuwa anataka kujua utekelezaji sasa wa hiyo ahadi ya Mheshimiwa Rais ambayo aliitoa, Rais akishatoa ahadi maana yake tayari ni amri kwetu sisi watekelezaji. Nimekwishamwambia kwenye jibu la msingi na jibu lake litakuwa ni hilo na hapa nitoe tu wito kwa ufupi hata kwa maswali ya nyongeza mengine kama inawezekana basi jibu litakuwa ni hilihili tu kwamba Waheshimiwa Wabunge wote wavute subira, wasubiri utaratibu huu ambao Serikali inaenda kufanya kwa kushirikisha Wizara nilizozisema ili twende tukatafute suluhu sasa ya matatizo haya kama nilivyokwishayasema.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, sisi suala la Pori la Mukungunero ni tofauti na maeneo mengine kwa sababu mauaji yamekwishatokea, maaskari watatu walikwishauawa pale, wananchi walishaandika barua mpaka kwa Waziri Mkuu na Waziri Mkuu akapeleka suala hili Wizara ya Maliasili lakini tangu mwaka 2013 suala la Mukungunero halijashughulikiwa. Naomba suala la Mkungunero sasa litazamwe kwa jicho lingine la haraka. Je, ni lini sasa Wizara ya Maliasili itaishughulikia barua iliyoandikwa kwao na Waziri Mkuu aliyepita?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, jibu fupi kabisa, naomba nimjibu Mheshimiwa Mbunge swali lake la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa maelezo aliyoyatoa ni wazi kwamba suala hili la Mkungunero, kwa jinsi swali lilivyoulizwa na uhalisia ulivyo lina upekee kama ambavyo na yeye ameweza kubainisha. Kwa hiyo, ushughulikiaji wa suala hili ndani ya Wizara ya Maliasili na Utalii unavuka mipaka, unahusisha masuala yanayohusiana na Wizara ya Mambo ya Ndani. Hapo unahusisha polisi na mambo mengine ya utendaji wa Kiserikali lakini nje ya mipaka ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Hata hivyo, kwa sababu ni suala linalohusiana na Wizara ya Maliasili na Utalii basi tutakwenda kuona namna ambavyo tunashirikiana na vyombo vingine ambavyo vinahusika katika kuweka msukumo kukamilisha ushughulikiaji wa changamoto hii.
AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kumuuliza Naibu Waziri maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, mapori ya akiba mengi yamegawanywa kwa leseni za uwindaji na uwindaji huu umekuwa unachangia katika kupunguza wanyama kwa maana ya kwamba wanyama wale wanauawa na ipo siku wanyama hawa wanaweza wakatoweka kabisa. Je, Serikali ina mpango gani wa kulitenga Pori la Akiba la Kigosi kuwa Hifadhi ya Taifa ili wale wanyama ambao wamekuwa wakipunguzwa sehemu nyingine wawe wanapata eneo ambalo watapata ulinzi wazaliane na kuongezeka ili waweze kusogea tena sehemu zile ambapo kuna leseni za uwindaji?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukiangalia Pori la Akiba ya Selous ipo Udzungwa National Park, ukienda Ruaha kuna Ruaha National Park na kuna Ruaha Game Reserve. Kwa maana hiyo, mimi nilikuwa nashauri kwamba ikiwezekana haya Mapori ya Kigosi/Moyowosi iwepo na sehemu nyingine ambayo itakuwa ni Hifadhi ya Taifa ambapo hawa wanyama watapata nafasi ya kuwa wanakwenda kuzaliana na kwenda kuongezeka kwa wepesi.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, napenda…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Masele, naomba ufupishe tafadhali, naona swali la kwanza ushauri wako umekuwa mrefu, swali la pili nenda straight kwenye swali.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, katika jibu lake la msingi amesema kwamba kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021, Serikali ina mpango wa kuimarisha miundmbinu. Je, Wizara yake itakuwa tayari sasa kutengeneza ile barabara ya kutoka Masumbwe kuelekea Kifura katika Wilaya ya Kibondo ili kuweza kurahisisha utalii wa ndani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la kwanza la utaratibu wa uvunaji na namna ya kuhakikisha kwamba uvunaji huu unakuwa endelevu ili usiathiri idadi ya wanyamapori kwa maana ya kufikia kiwango cha kumaliza baadhi ya aina (species) za wanyamapori, jibu lake ni kwamba utaratibu huo upo na ndiyo utaratibu unaotumika kitaalam. Utaratibu huo unaitwa quota, kwanza kuna aina maalum ya wanyama wanaoruhusiwa kuwindwa lakini pia kuna idadi maalum ya wanyama wanaoruhusiwa kuwindwa katika kipindi kinachotajwa kwa mujibu wa kanuni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na Kigosi/ Moyowosi, nimesema kwenye jibu la msingi kwamba tunalo eneo tunafanya utalii wa uwindaji lakini eneo lingine ni kwa ajili ya utalii wa picha. Sasa kule ambako tunafanya utalii wa picha ndiko maeneo ambayo tunatarajia kwamba kwa kutowawinda wanyama basi wataendelea kuzaana kama Mheshimiwa anavyoshauri lakini kwa ujumla ushauri tumeupokea na tutaufanyia kazi vizuri zaidi ili kuweza kuboresha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili la barabara aliyoitaja, labda niseme tu kwa ujumla kwamba tunapozungumzia miundombinu hasa miundombinu ya barabara kwa upande wa hifadhi, ziko barabara ambazo zinashughulikiwa moja kwa moja na Wizara ya Maliasili na Utalii na hizi ni zile ambazo ziko ndani ya maeneo ya hifadhi. Ukishatoka nje ya maeneo ya hifadhi unakutana na mfumo wa kawaida wa barabara Kitaifa ambapo utakutana na barabara zinazopaswa kutengezwa na Halmashauri za Wilaya husika lakini pia utakutana na barabara kuu. Miundombinu yote hiyo ni ya muhimu kwa sababu watalii hawawezi kufika kwenye hifadhi bila kusafiri umbali mrefu pengine wanatoka Dar es Salaam na maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Serikali itaendelea kuboresha miundombinu kama ya barabara, zile barabara kuu kupitia utaratibu wake wa kawaida wa Kiserikali wa kutengeneza na kuimarisha barabara hizo pamoja na zile za Halmashauri vilevile mpaka utakapofika ndani ya hifadhi. Zile za ndani ya hifadhi tunaendelea kuziboresha taratibu kadri fedha zinavyoweza kupatikana.
MHE. DOTO M. BITEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naomba nimshukuru sana Naibu Waziri kwa ushirikiano anaonipa kila wakati napoenda kumuona kwa mambo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimpe taarifa kidogo Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba lile zoezi la kuondoa wananchi kwenye msitu ule kama anavyosema kwamba walishirikisha Halmashauri si kweli nadhani kuna mahali fulani aliyempa taarifa hakusema ukweli.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Wilaya ya Bukombe eneo lake kubwa ni hifadhi na wananchi wanafuata huduma za maliasili Wilayani Kahama umbali wa kilometa zaidi ya 96. Je, Serikali haioni kuwa sasa muda umefika ifungue Ofisi ya Maliasili Wilayani Bukombe ili wananchi wanaofanya shughuli mbalimbali kama za kurina asali vibali vyao sasa wasihangaike kufuata Kahama ambako ni mbali sana?
Swali la pili, jambo lililotokea au tukio lililotokea Idosero linatishia vilevile vijiji mbalimbali ambavyo viko jirani, vijiji kama vile Nyakayondwa, Pembe la Ng’ombe, Kichangani, Matabe, Mwabasabi, Ilyamchele ambavyo viko Wilayani Chato vinatishiwa na jambo hili. Lakini vilevile kijiji kama vile Nyamagana, Ilyamchele vilivyoko kata ya Namonge, Wilaya Bukombe na vyenyewe wananchi wake hawajakaa kwa utulivu kwa sababu ya matishio haya haya. Serikali inawaambia nini wananchi hawa ili waweze kuishi kwa amani? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la umbali kutoka Kahama mahali ambapo wananchi hawa wa Bukombe wanakwenda kupata huduma zinazohusiana na masuala ya maliasili na ombi lake la kuletwa kwa kituo mahususi kwenye eneo la Bukombe au kwenye Wilaya ya Bukombe ili kuweza kurahisisha utekelezaji wa shughuli za maliasili, napenda tu kwanza nimhakikishie kwamba nia njema inaonyesha wazi kwamba si kuleta huduma tu peke yake bali pia hata kuiwezesha Wizara ya Maliasili na Utalii kuweza kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa sheria inayohusiana na suala la uhifadhi. Kwa hiyo, hilo ni jambo jema na ninalichukua na tunalipokea na tutalifanyia kazi ili kuweza kuona ni namna gani tunaweza kupata kituo kwenye eneo ambalo liko karibu na litakalowezesha wananchi kuweza kufika kwa karibu kutoka kwenye Wilaya ya Bukombe.
Kuhusu suala la vijiji jirani ambavyo vinaonekana kuwa na changamoto zinazofanana na zile tulizokutana nazo Idosero kwanza kwa kutamka tu kwamba ni vijiji maana yake ni kwamba ni vijiji vinavyotambuliwa kisheria na Serikali. Ukisema vijiji maana yake ni vijiji vya mujibu wa sheria na vimesajiliwa kwa hiyo, sasa kama nilivyotangulia kusema kwa upande wa Idosero. Kwamba kwa kuwa Idosero kama kitongoji ilipata GN chini ya Sheria ya Serikali na vilevile vijiji vilivyotajwa vilevile kwa kuwa ni vijiji uwepo ni kwa mujibu wa sheria basi nimesema sasa umefika wakati wa kwenda kuangalia sheria zote; hii ya maliasili na utalii na ile iliyoanzisha hivyo vijiji twende kuona namna gani tunaweza tuka-harmonize tuweze kupata suruhisho la kudumu, badala ya hizi operations ambazo zinazofanyika mara kwa mara na hazina majibu ya kudumu.
MHE. KANGI A. N. LUGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona kwa kuwa kwenye swali la msingi la Mheshimiwa Doto inaonyesha Wizara ina nguvu za kutosha za kupambana na wananchi ambao wanavamia maeneo ya hifadhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini sasa Wizara ya Maliasili itatmia nguvu hizo hizo kuzielekeza kwenye Ziwa Victoria kupambana na mamba ambao pia wamevamia wananchi wangu kuwala na wengine kuwajeuri ili kuhakikisha kwamba wanawavuna wasiendelee kuleta madhara kwa wananchi wa Mwibara?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza si sahihi sana kusema kwamba Serikali inatumia nguvu nyingi sana kwa maana ya matumizi ya mabavu wakati wa kusimamia sheria zake. Inawezekana hapa na pale watekelezaji wa sheria pengine huweza kufanya yale ambayo si sahihi sana. Lakini jambo la msingi sana kwa upande wa Serikali ni kusimamia sheria kwanza kwa kutoa elimu kuwaelimisha wananchi ili wasiweze kukiuka sheria na kuweza kutii sheria kwa hiyari huo ndiyo mwelekeo.
Lakini kuhusu suala la mamba wanaosumbua pengine wanaleta madhara ya wananchi kuuawa au kujeruhiwa hili ni suala ambalo limo pia kwa mujibu wa kanuni na taratibu upo utaratibu wa kufanya uvunaji kwa utaratibu ambao unatambulika kisheria na kisayansi na pale ambapo inaonekana kuna haja ya kuchukua hatua ambazo ni za dharura zaidi kuliko ule utaratibu wa uvunaji, basi utaratibu huo unaweza ukafuatwa. Sasa kwa kuwa ametaja eneo mahususi kule Ukerewe nalichukua na naliorodhesha na tutaenda kuangalia ni kwa kiwango tatizo hili la mamba linaleta matatizo kwenye eneo alilolitaja ili tuweze kuona kama tunatumia kanuni za kawaida za uvunaji ama tunaweza kulichukua kama suala la dharura na kuweza kwenda kuchukua hatua zinazostahili.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru huku nyuma hatuonekani inatubidi tuanze kunywa maji ya kutosha.
Swali langu kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, Rufiji tunabeba asilimia 49.8 la eneo la hifadhi na misitu nikimaanisha square kilometer 6,300 ziko ndani ya hifadhi na misitu, na kati ya hizo square kilomita 13,000 ndiyo eneo kubwa la Jimbo langu la Rufiji. Wananchi wa Jimbo la Rufiji wana masikitiko makubwa katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii ambapo hatujaingiwa katika mgao wa madawati.

Waziri, umetumia kigezo gani kugawa madawati katika maeneo ambayo wanatunza hifadhi ya misitu yetu naomba kufahamu hilo kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Rufiji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani inawezekana anazungumzia suala la mgao wa madawati uliofanywa hivi karibuni na Wizara kupitia TANAPA na kama hivyo ndivyo ningependa tu nimueleweshe tu kwamba TANAPA ni wasimamizi au wanashughulikia masuala ya uhifadhi, lakini kwenye hifadhi za wanyamapori siyo misitu. Na kigezo kilichotumika kwa kipaumbele ni kuangalia cha kwanza kuangalia maeneo yanayopakana na hifadhi hizo za wanyamapori tena zile ambazo ziko chini ya TANAPA hilo ni kuhusu swali hilo la mgao wa juzi. Lakini kwa upana wake ni kwamba kila wakati tutakapokwenda kuangalia sasa namna ambavyo jamii zinazoishi jirani na maeneo ya hifadhi au ya wanyamapori ni ilani ya Chama cha Mapinduzi, ni content ya ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba hawa wanaoishi jirani ndiyo wawe wanufaika wa kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama kwenye eneo hili la misitu anakokuzungumzia kule Rufiji hali ilivyo ni hivyo alivyosema basi nakwenda kutizama kama hivi karibu tumefanya uvunaji wa aina yoyote au kama hivi karibuni limejitokeza jambo lolote ambalo lina maslahi kwa wananchi niende kuangalia kama kulitokea kasoro ya kuweza kutowahusisha wananchi ambao amewazungumzia kwenye eneo lake. Na ikiwa hivyo ndivyo basi Serikali itachukua hatua za mara moja kurekebisha.
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, tangu kuanzishwa kwa pori hilo mwaka 1959 hadi sasa ni miaka 57; je, Serikali inaweza kusema kwa kipindi hicho, imepata faida gani zaidi ya Askari Wanyamapori kukodishia wafugaji na wakulima wasio na uwezo kuruhusiwa kulima halafu baadae wanagawana mazao?
Swali la pili, kwa majibu yaliyotolewa ninapata imani kuwa, Mheshimiwa Waziri anadanganywa na wataalam wa chini yake. Je, yuko tayari kuongozana na mimi kwenda kwenye Mbuga hiyo, ili akajionee changamoto zilizopo na baadae asiweze kudanganywa na watumishi wake?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza pori lina faida gani na zaidi ya miaka 50 iliyopita anataka kujua kuna faida gani imepatikana kutokana na uhifadhi huo?
Kwanza niseme tu kwamba faida za uhifadhi ziko zile ambazo unaweza ukazitazama kwa macho au ukazikamata mkononi ambazo ni za kifedha na pengine ni za kiuchumi moja kwa moja. Lakini uhifadhi hasa wa mapori wakati mwingine faida zake unaweza usizione kwa macho au ukakamata kwa mikono kwa sababu faida zake ni za kiikolojia zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, faida zake zinakwenda kuambukiza hata uwekezaji, hata shughuli zingine za kiuchumi, lakini pia hata uwepo wa dunia tunayoishi na nchi tunayoishi yakiwemo masuala ya hali ya hewa, upatikanaji wa maji, na mambo mengine ya namna kama hiyo. Kwa hiyo, faida zipo na ni nyingi, lakini kama alikuwa anakusudia za kiuchumi zinazohusiana na fedha, hilo ni suala la takwimu na kwa hiyo basi anaweza kutafuta fursa tukaonana na kwa kutumia wataalam ambao na wenyewe nitawasemea kwenye swali la pili basi tunaweza tukapata takwimu, kujibu vizuri zaidi kuhusiana na suala la faida za kifedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la kuongozana, kwanza niweke sawa juu ya suala hili ambalo linajirudia mara nyingi sana la kwamba kuna kupata taarifa ambazo ni za uongo au za kudanganywa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna jambo niko makini nalo ni hilo na naomba Waheshimiwa Wabunge mnisaidie ili kwa upande wangu lakini nafikiri kwa Serikali nzima; ikiwa kuna majibu ambayo yanakuwa yanatia mashaka na pengine ni ya uongo; kwa sababu majibu ya uongo ni kama vile yamedhamiliwa. Kama kunajitokeza mazingira kama hayo, basi tuanze sasa kukataa namna hiyo ya kufanya kazi, kwa sababu hiyo ni namna ambayo haifai.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa upande wangu anayetoa jibu ninamfahamu, na anapotoa jibu namuambia anaweka saini kabisa kwenye jibu hilo analonipatia. Sasa baada ya hili kwa sababu tayari umeishanipa hiyo indication baada ya hapa, mimi na yeye tutakwenda kutafuta jibu sahihi ni lipi kulinganisha na hili ili yule aliyelitoa sasa kama kweli amedanganya, kwa sababu kudanganya ni dhamira, basi atachukuliwa hatua kwa mujibu wa kanuni na taratibu, lakini kwa kawaida kila mmoja kila mtumishi wa Serikali, anao wajibu wa kutenda kazi zake sawa sawa na anao wajibu kwenye masuala ya kujibu maswali, anao wajibu wa kujibu maswali kwa niaba ya Serikali na kwa hiyo, anawajibika kutoa majibu ambayo ni sahihi.
MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nilikuwa naomba niulize Serikali na niulize Wizara ya Maliasili na Utalii, je, ni lini sasa italipa fidia au italipa kifuta jasho na kifuta machozi kwa wananchi katika hifadhi zote ambazo zinapakana na wanyamapori, leo ni mwaka wa tano fedha ambazo wananchi wamelipwa ukizingatia vijiji 16 Wilaya ya Babati Vijijini bado hawajalipwa wamelipwa shilingi milioni 12 tu kati ya shilingi milioni 100 na, na nikifuta jasho na wala siyo fidia.
Je, ni lini na ni lini sasa Serikali itakuja tulipendekeza hapa kwamba hifadhi husika ndiyo ziwe zinalipa hizo fidia badala ya Wizara ya Maliasili na Utalii ili iwe rahisi sasa hifadhi ambazo ziko jirani na hivyo vijiji waweze kulipa mara moja ili wananchi hao sasa wapate unafuu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru na naomba nijibu swali la nyongeza moja au mawili pengine inaweza kuwa moja kwa mawili kadri alivyouliza Mheshimiwa Mbunge.
NAIBU SPIKA: Ujibu moja tafadhali kwa sababu ndiyo kanuni zinavyosema kwa hiyo, chagua moja.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Ahsante, suala la ulipaji wa kifuta jasho na kifuta machozi, yapo mambo mawili jambo la kwanza ni utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa kanuni kwamba ule ni lazima utimie ukamilike na ambao unaanzia kwenye ngazi ya kitongoji au kijiji kwenda wilaya kwenda mkoa halafu kwenda hifadhi inayohusika na mpaka kwenye Wizara. Yale maombi au madai yanayopata sifa za kuweza kulipwa sasa yataingia kwenye kikwazo kingine cha pili ambacho si kikwazo lakini ni utaratibu kwamba kuna suala pia la bajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna suala la kutimiza vigezo halafu kuna suala la uwepo wa fedha. Sasa yale yanayohusiana na utaratibu kwa sababu unahusisha pia Wizara kama kuna madai ambayo yamekidhi vigezo lakini pengine yanachelewa kwa sababu tu ya procedure za kiofisi hayo tunakwenda kuongeza kasi kuharakisha ili yakae pending kusubiri uwepo wa fedha na fedha zitakapokuwa zimepatikana madai yote yanayohusiana na kifuta jasho, na kifuta machozi yatalipwa mara moja.
MHE. MARIA N. KANGOYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali yangu mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza Vyuo vya Utalii katika Mikoa mingine ya Tanzania hasa katika ngazi ya shahada? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa Mkoa wa Mwanza una makumbusho mbalimbali ya kihistoria yakiwemo ya Kageye na makumbusho ya kabila la Kisukuma yaliyopo Bujola Wilayani Magu, ambayo yamekuwa yakipoteza umaarufu wake kadri miaka inavyoongezeka. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba umaarufu huu wa makumbusho haya unaongezeka ili kuiwezesha Wilaya ya Magu kupata kipato kupitia utalii hasa tukizingatia kwamba Wilaya hii imekuwa na mapato madogo kiasi kwamba, imekuwa haikidhi haja ya utoaji wa asilimia kumi ya mapato yake kwa ajili ya vijana na wanawake?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza la kuongeza vyuo vya utalii na hasa katika ngazi ya shahada, napenda kutoa maelezo ambayo ndani yake kuna majibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, Serikali itaelekeza nguvu zake zaidi kwa sasa katika kuimarisha vyuo vilivyopo, vile ambavyo nimevitaja katika campus tatu, mbili zikiwa Dar es Salaam na moja ikiwa pale Arusha.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunazingatia kuongeza vyuo zaidi, tutazingatia pia ukweli kwamba kitaalam na hasa unapozungumzia kuongeza mafunzo hayo katika ngazi ya shahada ili wahitimu wenye ngazi ya Shahada waweze kufanya kazi sawasawa na yenye tija, unahitaji zaidi kuwa na wataalam katika ngazi ya kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutaelekeza nguvu zetu zaidi kwa wataalam wa ngazi ya kati sambamba na kuangalia uwiano kati ya wale wahitimu wanaohitimu katika vyuo vya kati ili tuweze kuboresha zaidi utendaji wa wale ambao watakuwa wamehitimu katika ngazi ya shahada hapo baadaye, lakini kwa sasa hivi tuelekeze nguvu nyingi zaidi katika kuzalisha wataalam katika ngazi ya kati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la makumbusho yaliyoko katika Mkoa wa Mwanza na umaarufu wake unaoendelea kupungua, namwomba Mheshimiwa Mbunge arejee majibu ya maswali yaliyotangulia hapo awali. Hata hivyo, nitarudia pia kwa ufupi kwamba, hivi sasa mpango wa Serikali kupitia Wizara ya Wizara ya Maliasili na Utalii ni kwenda katika kila Halmashauri ya Wilaya nchini na kuorodhesha aina zote za vivutio vya utalii ikiwemo makumbusho mbalimbali ili tuweze kupanga vizuri zaidi namna ya kuweza kuvitunza vile vilivyopo katika hali iliyopo, kuviboresha na kuweza kuvifanya viweze kuchangia vizuri katika uchumi wa Taifa kwa kadri ambavyo tutaweza kuvitangaza zaidi.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ni Wilaya yenye vivutio vingi vya kitalii na vijana wa Lushoto wanafanya kazi ile kwa mazoea. Je, ni lini Serikali itafungua Chuo cha Kitalii ili kuwajengea uwezo vijana wa Lushoto ili wasifanye kazi ile kwa mazoea?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawapongeza vijana wa Lushoto kwa moyo wao wa kujitokeza kupenda kufanya kazi katika eneo hili, kwa sababu kupitia kwao, tutaweza kufanya ajira kwa vijana ikawa imepata mchango mkubwa sana kupitia Sekta ya Utalii na kupitia kwao tunaweza kuchangia vizuri zaidi uchumi wa Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kufanya kazi kwa mazoea na mahitaji ya kupata mafunzo, kwanza nipate takwimu kwa sababu kwa sasa hivi Mheshimiwa Mbunge ametoa maombi ambayo ni ya jumla, nimtake sasa tuweze kushirikiana, nione kwamba kwenye eneo la Lushoto lile kuna vijana wangapi ambao wamejitokeza kupendelea kuingia katika fani hii. Kwa sababu ninachoamini ni kwamba vyuo tulivyonavyo bado havijaelemewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa taarifa zilizopo mpaka sasa hivi, vyuo tulivyonavyo bado vina uhitaji wa wanafunzi; lakini kama itajitokeza kwamba vyuo vinalemewa na kuna uhitaji wa kuongeza vyuo vingine, au kuboresha mazingira ya vyuo vilivyopo ili viweze kupokea wanafunzi zaidi, basi Serikali itaweza kuchukua hatua muafaka ili kila mmoja mwenye nia na kiu ya kujiunga kwenye mafunzo yatakayompelekea kuwa na taaluma muhimu ya kushiriki vizuri zaidi kwenye Sekta hii ya Utalii aweze kufanya hivyo bila mashaka yoyote.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa nchi yetu kiutalii na kitakwimu tunaambiwa ni nchi ya pili kwa kuwa na vivutio baada ya Brazil na ili kunufaika zaidi na utalii ambao tunaambiwa pia kitakwimu ndiyo sekta zinazoongoza kwa kuingiza fedha za Kigeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kusudi kuiwezesha Bodi ya Utalii Tanzania kufanya promotion na advertisement kwa kiwango cha kuridhisha na hivyo kuongeza idadi ya watalii; je, Serikali iko tayari sasa kuunda chombo maalum ambacho kitasimamia ile Tourism Development Levy kusudi kuiwezesha TTB kufanya promotion na advertisement kwa kiwango kikubwa ili kuvutia watalii wa kutosha na hivyo kuongeza mapato ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli na nafikiri hapa anatukumbusha tu; kama ambavyo nimesema mara nyingi, nchi yetu ina vivutio vingi vya utalii; na ni ya pili baada tu ya Brazil. Kuhusu suala la Tourism Development Levy (TDL) namna ambavyo inaweza kuchangia zaidi na inavyoweza kusaidia zaidi Bodi ya Utalii, (Tanzania Tourism Board) kufanya majukumu yake vizuri zaidi na wazo la kuanzishwa kwa chombo kingine tena cha kuweza kusimamia TDL, napenda kujibu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi, suala la (Tourism Develeopment Levy - TDL) kama lilivyo, halina matatizo yanayohitaji kuanzishwa kwa chombo kingine kusimamia. Tunahitaji kuboresha vizuri zaidi usimamizi kupitia vyombo vilivyopo chini ya Serikali hivi sasa, lakini ni kweli kwamba tunakwenda sasa kujipanga vizuri zaidi ili mapato yanayopatikana kutokana na Tourism Develepment Levy yaweze kusaidia zaidi Bodi ya Utalii kutimiza majukumu yake ambayo kwa kiwango kikubwa ni kutangaza utalii ndani na nje ya mipaka ya nchi hii kwa ajili ya kuboresha mapato ya Taifa kupitia Sekta ya Utalii.
MHE. HAFIDH ALI TAHIR: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake sahihi, lakini nina maswali madogo ya nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri, anataka kuliambia Bunge hili kwamba suala la Kampuni ya Zululand kwamba ni ya Afrika Kusini ni kauli ya upotoshwaji kwamba inamiliki Kisiwa hiki?
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri atuambie, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kati ya utalii Zanzibar na ile ya Muungano, wanashirikianaje katika suala zima la utalii katika ulimwengu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ni kweli kama nilivyofafanua kwenye jibu langu la msingi kwamba Kisiwa cha Shungimbili na kazi inayofanyika hivi sasa pale, kwa ujenzi wa ile hoteli ya Kitalii, ile lodge; inaendelea kufanyika chini ya MPRU ambayo iko chini ya Wizara ya Kilimo na Uvuvi, kazi hiyo itakapokamilika, itakapoingia sasa kwenye masuala ya uwekezaji yenyewe; ya uendeshaji wa biashara yenyewe ya hoteli; pale sasa ndiyo Wizara ya Maliasili na Utalii inapoingia, watakapokuja sasa kuomba Leseni ya Biashara ya Utalii ambapo sasa watalazimika kuomba leseni hiyo chini ya chombo chetu cha Tanzania Tourism Licencing Board. Pale tutaweza sasa kutoa hiyo leseni, ikiwa watakidhi vigezo vyote ambavyo vipo kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ushirikiano kati ya Bara na Visiwani, ni kama nilivyojibu kwenye swali la msingi na niliorodhesha masuala kadhaa ambayo tunayafanya kwa kushirikiana baina ya pande zetu zote mbili za utalii. Kwa faida ya Mheshimiwa Mbunge mwuliza swali pamoja na Wabunge wengine, nimesema ushirikiano kati ya pande mbili za Muungano, unajumuisha maeneo ya utangazaji wa vivutio vya Tanzania Kimataifa kama nchi moja, utayarishaji taarifa na ujenzi wa mfumo imara wa ukusanyaji wa takwimu ambapo takwimu hizo sasa ndiyo zinatumika Kimataifa kwa ajili ya kuifahamu vizuri zaidi nchi yetu na masuala yanayohusiana na utalii, kwa sababu ni takwimu zinazohusiana na utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimetaja hayo mawili miongoni mwa manne ambayo nimekwishayataja, lakini mtu anaweza kurejea kwenye jibu langu la msingi kwamba hayo ndiyo maeneo ambayo tunafanya ushirikiano au mashirikiano baina ya pande hizi mbili za Muungano.
MHE. MARTHA M. MLATA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Ningependa tu kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba kwa kuwa hoteli hizi ambazo ni maalum sana, ambazo zinaitwa ‘za Kimataifa’, zinazojengwa kwenye maeneo maalum, zimekuwa zikichukua ajira za wafanyakazi wengi kutoka nje, zile ambazo ni muhimu sana na kuwaacha wazawa wakifanya kazi zile ndogo ndogo kwenye hayo mahoteli makubwa. Je, Serikali inajipanga vipi kuhakikisha kwamba nafasi zile kubwa zinachukuliwa na wazawa kuliko wafanyakazi kutoka nje?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kwa ufupi kabisa! Ukweli ni kwamba mfanyabiashara anapotafuta mtu wa kumwajiri ili aweze kutoa huduma katika eneo lake la biashara, lazima atakuwa anatafuta mtu ambaye atamwezesha kupata tija katika biashara yake. Kwa hiyo, hilo linakuwa ni suala la ushindani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeliona jambo hili kwamba kwa upande wa nchi yetu, tunao upungufu kwa kiwango fulani juu ya kuweza kushindana katika masoko haya ambayo yanahusisha ushindani wa Kimataifa. Kwa hiyo, hatua ya kwanza ambayo tutaifanya ni ile ambayo tunaboresha zaidi Vyuo vyetu ili tuboreshe zaidi wananchi wetu, waingie, wajifunze; lakini siyo kujifunza tu darasani, wakitoka pia waweze kufanya kama walivyojifunza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengine, kwa mfano ya hospitality ni zaidi hata ya kujifunza darasani, lakini pale ni lazima mtu uweze ku-gain competencies ambazo zitaweza kukuwezesha kupambana kwenye soko la ajira; lakini haitafikia wakati tukaweza kumlazimisha mfanyabiashara kumwajiri mtu; isipokuwa tutajenga mazingira ya kuwawezesha Watanzania wawe washindani wazuri zaidi.
MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Kwa kweli ni miongoni mwa Mawaziri ambao wanatoa majibu ambayo hayana ukakasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba niulize swali dogo la nyongeza. Pamoja na maboresho hayo lakini kumekuwa na malalamiko kuhusu wale wapagazi kunyanyasika kwa kulipwa kiwango kidogo. Je, ni lini Seikali itaweka utaratibu wa kuboresha maslahi yao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sikudhani Chikambo, Mbunge wa Viti Maalum kutokea Mkoa wa Ruvuma, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimesema kwenye majibu yangu ya swali la msingi, kwamba tutaboresha hali za wafanyakazi wanaotoa huduma kwenye sekta ya utalii kwa ujumla wake na wapagazi ni sehemu yao. Watalii wakifika kufanya utalii katika nchi yetu mojawapo ya vitu vitakavyofanya wao wanaofika kwanza waendelee kubaki kwa muda mrefu zaidi lakini pia kuweza kuvutia watalii wengine kuja ni pamoja na aina ya huduma wanazozipata na huduma hizo zinatolewa na wale ambao wamepewa fursa hiyo na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuboresha mazingira ya watenda kazi hawa ni jambo la msingi na Serikali inalizingatia ili kwa kufanya hivyo tuweze kuvutia watalii zaidi na wakija waweze kukaa kwa muda mrefu zaidi kwa ajili ya tija ya mapato kwenye sekta ya utalii.
MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa askari wengi wa wanyamapori huwa wanapata athari ama wanafanya kazi katika mazingira magumu ya wanyama wakali. Je Serikali inawafidia nini wale askari wa wanyamapori ambao wanaathiriwa na wanyamapori wakali?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Faida Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze kwa kuwa imekuwa ni jambo la kawaida na linalojitokeza mara nyingi sana tunapowazungumzia askari wa wanyamapori tunazungumzia juu ya yale ambayo si ya maslahi zaidi kwao na mara nyingi ni lawama tu juu ya utendaji wao wa kazi. Kwa hiyo, kutokana na mwelekeo huu mpya wa Mheshimiwa Faida Bakar wa kuona kwamba na askari wa wanyamapori na wenyewe wana haki zao na maslahi yao yanapaswa kuboreshwa kutokana na kazi ngumu wanayoifanya natoa pongezi juu ya hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kujibu swali lake ni kwamba kwa mujibu wa kanuni na taratibu za ajira zilizopo na kwa mujibu wa sheria maslahi au haki za wafanyakazi hawa ambao ni askari wa wanyamapori zinazotokana na mazingira yao ya kazi zimezingatiwa. Ili kuongeza tija kwenye eneo hili huko tuendako na mkakati wa Kitaifa wa kuboresha zaidi ulinzi wa rasilimali zetu, Serikali inao mpango wa kuboresha hali na mazingira ya kazi hii ikiwa ni pamoja na ulipaji wa fidia, vifuta jasho pamoja na vifuta machozi kwa namna ambavyo itaonekana inafaa. Tutapitia utaratibu huo ili kuboresha mazingira na kuongeza ari zaidi kwa wafanyakazi wetu ikiwa ni pamoja na askari wa wanyamapori.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WATU WENYE WALEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini naomba nilipe taarifa Bunge lako Tukufu kwamba Serikali kupitia Bunge hili limeshapitisha Mfuko wa Fidia kwa wafanya kazi wote wanaoumia katika nchi yetu ya Tanzania wakiwa kazini. Mfuko huu ni kwa wafanyakazi ambao wapo kwenye private sector na wafanyakazi ambao wanafanya kazi ndani ya Serikali yetu. Katika Mfuko huo utaratibu umewekwa ambapo waajiri sasa wameanza kuchangia na pale ambapo mfanyakazi anapoumia kazini akiwa sekta binafsi ama Serikalini Mfuko huo sasa una jukumu la kulipa fidia kwa kuzingatia kanuni na taratibu zilizowekwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niwahakikishie Wabunge, Ofisi ya Waziri Mkuu imeanza kusimamia utaratibu huo. Mfuko huo utaanza kazi hiyo mwaka huu ili kuweza kutatua tatizo la wafanyakazi wengi wanaoumia kazini wakiwemo hao askari wa wanyamapori pia.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nimeona katika jibu la msingi la Naibu Waziri amesema viongozi wa vijiji vya Ngorongoro hawakutoa ushirikiano. Nataka kufahamu, kama viongozi hao hawakutoa ushirikiano ina maana Serikali ndiyo imekata tamaa? Kwa sababu wananchi wale wamekuwa wakipata shida sana, nyumba zao zimekuwa zikichomwa moto na mifugo yao imekuwa ikiuliwa. Nataka jibu la Serikali kuhusiana na kumaliza mgogoro huu wa Ngorongoro. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa migogoro mingi imekuwa ikichangiwa na wafanyakazi wa wanyamapori. Je, Serikali inawachuja vipi maafisa wake wale wasiokuwa na maadili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la kwanza kama Serikali imekata tamaa au laa, jibu la moja kwa moja ni kwamba, Serikali haijakata tamaa na wala Serikali haiwezi kukata tamaa katika kushughulikia changamoto ambazo zinawahusu wananchi wake. Kwa nyongeza tu ni kwamba, kwenye jibu langu la msingi nimetaja wilaya ambazo zinahusika na mgogoro ukizihesabu ni wilaya saba.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika wilaya sita mgogoro huu ulishughulikiwa baada ya kupata ushirikiano mzuri kutoka kwa wananchi na Serikali zao za Wilaya na Wizara ya Maliasili na Utalii. Changamoto zilizojitokeza kwenye vijiji hivi vya Wilaya ya Ngorongoro ni kama hivyo nilivyozieleza lakini kama nilivyotangulia kusema hapo awali tumeuorodhesha mgogoro huu ambao unahusu vijiji hivi vya Wilaya ya Ngorongoro kuwa miongoni mwa migogoro ya hifadhi ambayo haijashughulikiwa kikamilifu na nimesema Serikali inaenda kumaliza changamoto hizo katika zoezi linaloenda kufanyika hivi karibuni kimkakati zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili linalohusiana na wafanyakazi wa wanyamapori, nashukuru ameweza kuweka vizuri kabisa kwamba ni baadhi ya wafanyakazi. Jambo la kwanza kabisa wako wafanyakazi walio wengi wa wanyamapori wanafanya kazi zao kwa uadilifu mkubwa na kwa kuzingatia maadili, miiko, kanuni na taratibu na miongozo ya kazi zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale wafanyakazi wachache ambao wanatumia vibaya nafasi zao, kwa kutumia mwanya wa kutekeleza sheria kwa kuvunja sheria na kufanya vitu ambavyo ni kwa kinyume kabisa na kanuni na taratibu hao wanafanya hivyo wakiwa wanavunja sheria. Kwa hiyo, sasa tunajipanga zaidi kwenda kuwashughulikia mmoja mmoja na kwa makundi ili waweze kukomesha kabisa tabia hiyo na wananchi waweze kutii sheria kwa kuongozwa na kanuni na taratibu na sheria zenyewe badala ya matumizi mabaya ya sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitumie tu fursa hii pia kutoa wito kwa askari wote wa wanyamapori kwa ujumla wao kwamba wale ambao hawahusiki na vitendo hivi vibaya watumie nafasi zao kuwashauri wenzao lakini wale ambao wana tabia hii wakumbuke tu kwamba katika Serikali ya Awamu ya Tano mambo ya kufanya kazi kwa mazoea, kwamba ulikuwa unafanya namna fulani ulivyozoea tangu huko nyuma sasa imepitwa na wakati na sasa tumefungua ukurasa mpya kabisa wa kutaka kwenda kufanya vitu kwa mujibu wa kanuni na taratibu. Wajiepushe na taratibu za kujificha nyuma ya pazia la utekelezaji wa sheria kuonea wananchi kwa kuwachomea nyumba moto, kuwapiga na vitendo vingine vyote visivyofaa.
MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Katika Jimbo la Nkasi Kusini kuna Mbuga ya Wanyama inaitwa Rwamfi Game Reserve. Pamekuwepo na migogoro baina ya mipaka yake na Vijiji vya Ng’undwe, Mlambo, King’ombe Kasapa na vinginevyo. Katika michango mingi nimekuwa nikiuliza maswali lakini pia katika mchango wa Wizara hii niliweza kuorodhesha vijiji hivi kwamba vina mgogoro. Je, Waziri anafahamu kwamba mgogoro upo na ni miongoni mwa orodha iliyokwishamfikia kwa ajili ya kusuluhisha migogoro hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme tu kwa ujumla kwamba katika migogoro ya ardhi ambayo Serikali imekwishaorodhesha, yote kwa ujumla ni migogoro takribani 289. Miongoni mwao ambayo inahusiana na masuala ya uhifadhi ni migogoro 35, ukifanya hesabu ya haraka pale ni kama asilimia kumi na mbili na nusu ya migogoro yote ya ardhi nchi nzima inahusu uhifadhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro alioutaja kwenye eneo lile jirani kabisa na Katavi kule ni miongoni mwa migogoro ambayo imeorodheshwa kwenye orodha ya migogoro ya hifadhi ambayo tunakwenda kuishughulikia. Naomba nimshauri Mheshimiwa Mbunge baada ya kipindi hiki tuonane ili kwanza nimthibitishie kwamba migogoro hiyo ni miongoni mwa ile iliyoorodheshwa halafu asubiri hatua ambazo Serikali inachukua kushughulikia migogoro yote inayohusiana na masuala ya uhifadhi.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Hali ya migogoro iliyoko Serengeti na vijiji vya Ngorongoro inafanana na hali iliyopo katika Wilaya yangu ya Mkinga eneo la Kimuni katika mpaka wetu na Kenya na Pori Tengefu la Umba na Mbuga ya Mkomazi. Wananchi kwa muda mrefu wameomba mgogoro huu ili utatuliwe eneo lile litangazwe kuwa WMA lakini kwa muda mrefu hatujapata majibu, nini suluhisho la jambo hili na Waziri anatuambia nini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao wanaishi kwenye maeneo yanayopakana na hifadhi kila mmoja kwa wakati wake tuweze kupata nafasi ya kuwasiliana ili tuweze kuangalia maeneo yake ambayo anaona yana mgogoro ni kweli yameorodheshwa kwenye orodha ninayoizungumzia ambayo imetayarishwa na Serikali. Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kujibu swali mahsusi la Mheshimiwa Dunstan Kitandula kuhusu eneo la Kimuni, Umba, Mkomazi na hasa kuhusiana na suala la maombi ambayo wameyaleta Serikalini kwa ajili ya kuundwa kwa WMA. Ni kweli WMA inaundwa kwa makubaliano baina ya wananchi wa eneo linalohusika na Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii. Sasa nimpe tu comfort Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa suala hili ni mahsusi itakuwa ni vigumu kukumbuka maombi haya kama yameshatufikia tayari na yako kwenye status gani kwa sasa, nimuombe baada ya kikao hiki mchana tuweze kuwasiliana kwa sababu wakati huo mimi nitakuwa nimewasiliana na ngazi zinazohusika ili kuweza kupata uhakika zaidi ya majibu ya status au hatua gani imefikiwa kuhusiana na maombi ya WMA kwenye maeneo anayoyazungumzia.
MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, Jimbo la Mlimba na Jimbo la Kilolo ni majimbo yanayopakana. Kwa kuwa vijiji vingi ambavyo vinapakana na hifadhi huwa haviruhusiwi kufanya shughuli zozote za kibinadamu ndani ya hifadhi lakini tembo wamekuwa kero kwenye vijiji hivyo, kwa mfano, Kata ya Ruaha Mbuyuni, Mahenge na Nyanzo hivi ninavyozungumza uharibifu mkubwa wa mazao umefanyika. Je, Serikali itakuwa tayari sasa kutoa tamko lolote leo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la wanyama waharibifu kuvamia mashamba, ni kweli Serikali inazo taarifa kutoka katika vijiji mbalimbali vinavyopakana na hifadhi juu ya usumbufu wa wanyamapori wanaoharibu mazao ya wananchi. Siku za nyuma tulikuwa tukijikita zaidi katika kutumia vikosi vya Askari wa Wanyamapori kupambana na wanyama hao, lakini pale inapotokea wameshafanya uharibifu tulikuwa na ule utaratibu wa vifuta jasho.
Hata hivyo, Serikali imeshaona kwamba kutumia vikosi tu vya Askari wa Wanyamapori nguvu hiyo haitoshi lakini pia kusubiri mpaka wanyama wawe wameshafanya uharibifu ndipo tulipe vifuta jasho nao pia siyo mkakati mzuri kwa sababu siyo endelevu wakati mwingine gharama zinakuwa kubwa kuliko bajeti ya Serikali. Kwa hiyo, kuanzia sasa Serikali imejipanga upya kubadilisha ulinzi ule wa kutegemea tu Askari wa Wanyamapori na kwenda kwenye ulinzi shirikishi au kufanya uhifadhi shirikishi. Vijiji vyote vinavyopakana na hifadhi kutapatikana askari ambao watawezeshwa kwa kupewa elimu na silaha kwa utaratibu ambao utaonekana unafaa ili ulinzi sasa ufanyike kwa njia ambayo ni pana zaidi ili kuweza kuzuia zaidi kuliko kusubiri kutibu baada ya kutoa vifuta jasho
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, japo hayaridhishi sana, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa miti ya asili huwa ukuaji wake siyo wa kasi na wameshaanza kupanda miti katika hizi hekta 11, kwa nini wasione umuhimu wa kumalizia hizi hekta 38 ili ku-cover eneo hili la msitu kwa sababu msitu huu una vyanzo zaidi ya vinne vya mito ambayo inatiririsha maji kuelekea katika mbuga ya Mkomazi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mvua za mwaka jana, zilisababisha uharibifu mkubwa kutokana na maporomoko yaliyosababisha uoto wa msitu kupotea, hivyo kusababisha uharibifu mkubwa katika barabara za Kata ya Shagayu, Mbaramo na Sunga. Je, Wizara haioni sasa kuna umuhimu wa kipekee wa kuwaunga mkono wakazi wa maeneo haya ili kuweza kuboresha miundombinu hii ya barabara iweze kusaidia hata wakati mwingine wanapakuwa na dharura za moto waweze kufika katika eneo husika kwa haraka zaidi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze kwa kutambua kwamba misitu inachangia kiasi kikubwa au ndiyo msingi kwa kweli wa kuweza kuboresha vyanzo vya mito. Ana mito minne, na kwamba yote minne chanzo chake kikubwa ni misitu hii tunayoizungumzia.
Kwa hiyo, kwa kutambua hivyo nampongeza lakini nataka elimu hiyo pia aweze kuifikisha kwa wananchi kwenye eneo lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali kwa nini sasa tusipande miti kwenye lile eneo ambalo lina hekta 38 tulizosema tuache miti ikue kwa utaratibu wa asilia. Kwanza, nimfahamishe tu kwamba, mimea ikiwemo hiyo miti kwa kawaida huwa kuna mimea ambayo ni rafiki kukua pamoja na mimea mingine si rafiki kukua kwa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo lake siyo baya lakini tunapaswa kufanya kwanza utafiti wa kitaalam, na nitafanya utaratibu wa kufika kwenye eneo lile na wataalam ili tuweze kuona miti iliyopo ni miti gani inayotakiwa kukua asilia, halafu tuone kama kuna miti rafiki inayoweza kupandwa ilimradi tusichague miti ambayo itaathiri ile miti ambayo inatakiwa kukua asilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, uwepo wa barabara ambazo zinasaidia kutumika wakati wa dharura za moto na matumizi mengine ambayo ni rafiki kwa utunzaji wa misitu.
Kwanza ni dhahiri kwamba hiyo pia ni interest yetu pia sisi kama Serikali, lazima tuwe na barabara ambazo zinaweza kutusaidia wakati wa dharura kama moto utatokea, na kuwa ni jukumu letu kushirikiana na wananchi, na mamlaka za Wilaya zilizopo kuweza kuhakikisha kwamba barabara hizi zinatengenezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni suala la kuangalia hali ya kibajeti, lakini pamoja na hayo katika safari hiyo nitakayokwenda nitakwenda pia kuangalia hali ya barabara na kuweza kuona namna gani tunaweza kuweka kwenye mipango yetu.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Kwa miaka mingi sana nchi yetu imekuwa ikihamasisha sana utalii kupitia Mbuga zetu za Wanyama, Mlima wetu na Mapori yetu, lakini nchi ina vivutio vingi sana. Sasa nauliza; je, Wizara ina mpango gani wa kujenga makumbusho ili vizazi vyetu viweze kujionea jinsi Machifu wetu kwa mfano Mirambo, Mkwawa, kule Kilimanjaro, Mshumbue Marialle ambao walifanya vitu vingi na kuna vitu vingi vya asili vinavyoweza kuvutia utalii, kule Kusini, Wilaya ya Kilwa ni Wilaya ya zamani sana elfu moja mia nane na kitu, lakini vivutio vyote hivi havizungumzwi.
Je, Wizara ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba inajenga makumbusho ili vivutio hivi viweze kuwa kwa faida ya watoto wetu kwa kujifunza na vilevile kutuingizia fedha kutokana na watalii kutoka nje?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze kwa kuweza kutupa hamasa sisi Serikali, hasa upande wa Wizara ya Maliasili na Utalii, kuongeza jitihada kwenye Sekta hii ya Utalii. Ni kweli na nipende tu kusisitiza kwamba, majukumu manne makubwa ya Wizara ya Maliasili na Utalii, pamoja na utalii wenyewe ni misitu, wanyamapori na malikale.
Makumbusho anayozungumzia Mheshimiwa Mbunge yanaangukia kwenye sehemu ya malikale na imo kwenye sera zetu kwamba tunapaswa kuboresha makumbusho maeneo yote ya kihistoria popote pale yalipo ili tuweze kuyatangaza na kuweza kuwafanya watalii waweze kuyafikia pamoja na kutupatia pesa, lakini pia kuweza kutangaza utamaduni wa Mtanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokifanya kwa sasa tumeanza kuorodhesha katika ngazi ya Wizara, pia hivi karibuni tunasambaza barua kwa Halmashauri za Wilaya zote ili waweze kutuambia kwa sababu wao wanafahamu vizuri maeneo hayo halafu tutakwenda kuyakagua kuona kama yatakidhi vigezo vya kuweza kuyafanya kuwa ni maeneo ya utalii.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, upandaji wa miti ndiyo hasa unaoleta uoto wa asili; Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wananchi wa Lushoto katika upandaji wa miti hasa maeneo ya msitu wa Magamba, Mazumbai ili kurudisha uoto wa asili uliotoweka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea wazo lake na kwa kweli ni msisitizo kwa kile ambacho Serikali inakifanya, lakini na yeye sasa nimwombe arudi kule kwa wananchi aanze kuwashawishi kwa kuwaelewesha kwanza umuhimu wa misitu, lakini pia kuwafanya wajipange kwa ajili ya kupanda miti ili kuungana na jitihada za Serikali ambazo tayari zipo kwenye mipango.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishatoa maelekezo kwa Wilaya na Mikoa yote kwamba kila Wilaya inalazimika kupanda miti 1,500,000. Kabla ya msimu wa kuanza kupanda kila Wilaya, sasa inawajibika kuhakikisha kwamba inaandaa mbegu, vitalu na kuhakikisha kwamba miche ya kupanda kila eneo inapatikana. Kwa sasa hivi sisi Wizara tunahakikisha tunawapelekea maelekezo ya kila eneo miti gani inayoota na inayoweza ku-survive bila matatizo. Kwa hiyo, kila Wilaya wanalo jukumu hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ndani ya Wizara ya Maliasili pamoja na hii Ofisi ya Mazingira kwa maana ya Ofisi ya Makamu wa Rais, tutaendelea kusaidia pale inapobidi lakini ni mkakati wa kila Wilaya na Mkoa kuhakikisha kwamba kila Wilaya inapanda miti hiyo kwa mwaka inapofikia kipindi husika.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Pamoja na majibu yaliyotolewa na Serikali ambayo kimsingi sijaridhika sana, naomba kwanza niifahamishe Serikali kwamba maporomoko ya Kalambo ni ya pili Afrika yakifuatiwa na maporomoko ya Victoria. Kwa hiyo, yana unyeti na upekee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuifahamisha Serikali, naomba nimkumbushe Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba mazungumzo yalikuwa yameshaanza kati ya Halmashauri ya Kalambo na TANAPA wakijua umuhimu wa maporomoko haya. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kuhakikisha kwamba anayasukuma mazungumzo haya na ili maporomoko ya Kalambo yapandishwe hadhi na kuchukuliwa na TANAPA? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa maporomoko ya Kalambo yapo mpakani mwa Tanzania na Zambia na wenzetu wa upande wa Zambia wamekuwa wakiyatumia na kuyatangaza maporomoko haya na wakinufaika pamoja na kwamba scenery nzuri iko upande wa Tanzania. Je, Serikali iko tayari kuweka mkakati mahsusi kuhakikisha kwamba maporomoko haya yanafanyiwa promotion ya pekee?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza la mazungumzo yaliyokwishafanyika awali kati ya TANAPA na Halmashauri ya Wilaya inayohusika lakini akihusianisha na umuhimu wa maporomoko haya yakiwa ni ya pili kwa ukubwa na umaarufu katika Afrika, napenda niungane naye kusema kwamba mazungumzo yakianza ni sharti yakamilike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimfahamishe pia kuhusu kuwa maporomoko haya ni ya pili kwa ukubwa na umaarufu Afrika, Wizara inayo taarifa hiyo. Hata hivyo, nimfahamishe tu kwamba, tukisema bado yatasimamiwa chini ya Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) haimaanishi kwamba tunayashusha hadhi wala haimaanishi kwamba tutapunguza kasi na nguvu ya kuyatangaza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kuwa nimesema kwamba suala hili ni kwa mujibu wa sheria, Hifadhi za Taifa zina tafsiri yake kama ambavyo nimesema hapo awali na kwamba misitu ama maporomoko haya ambayo yapo ndani ya msitu tuliouzungumzia kwa mujibu wa sheria iliyopo sasa hivi yenyewe hayawezi kuwa Hifadhi ya Taifa kwa sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikubaliane na Mbunge kwamba nakwenda kufanya rejea ya mazungumzo yaliyokwishafanyika kwamba nini kilizungumzwa, tuliamua nini hapo nyuma ili kutotoka nje ya mazungumzo, lakini kwa sasa hivi mpaka nitakapokwenda kuona mazungumzo hayo msimamo ni kwamba, Hifadhi za Taifa zitabaki kuwa Hifadhi za Taifa na misitu itabaki kuwa misitu na itasimamiwa kwa sheria zinazohusika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili la kuweza kufanya promotion ya pekee, hili nakubaliana nalo moja kwa moja na namwomba Mheshimiwa Mbunge nikitoka hapa hebu tukutane, inawezekana ana maoni mazuri zaidi kuliko hiki ambacho Serikali imefanya. Nakiri kabisa siyo tu kwa maporomoko haya bali kwa ujumla wake kutangaza vivutio vya utalii ni jukumu la Serikali na kwamba tunapaswa kuboresha namna ambavyo tumekuwa tukifanya siku zote ili tuweze kufanya vizuri zaidi ili vivutio vyetu viweze kufikiwa na watalii kwa wingi na kuongeza pato la Taifa.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, wakati Jumuiya inaanzishwa maeneo haya yalikuwa na kijiji kimoja tu cha Sibwesa, lakini leo hii kuna vijiji zaidi ya sita na kata mbili zimeanzishwa kwenye maeneo hayo na Serikali inatambua maeneo hayo ya kiutawala. Je, ni lini Serikali kupitia Wizara wataenda ku-review mipaka hiyo ambayo ipo inayoleta migogoro ya mara kwa mara kwenye maeneo hayo ili kuondoa shida inayosababisha wananchi kupigwa mara kwa mara? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, wakati Jumuiya inaanzishwa ilikuwa na malengo mazuri ya kiuchumi ambayo kwa sasa hayapo na wananchi hawajanufaika na mradi wowote ule ulioanzisha Jumuiya hiyo. Je, Serikali ina mpango gani wa kuyaachia hayo maeneo ili yaendelezwe na vijiji vyenyewe husika?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza kimsingi anakubaliana na hoja ya jibu la msingi kwamba tangu wazo la kuanzishwa kwa WMA lilipotolewa hadi leo mabadiliko mengi yametokea ikiwemo kuongezeka na kubadilika kwa maeneo ya utawala. Ameuliza swali ni lini Serikali itaenda kushughulikia mabadiliko hayo na kuweza kupima umuhimu wa kuendelea na wazo la WMA?
Mheshimiwa Spika, jibu langu ni kwamba mara tu baada ya kukamilika kwa kikao hiki kinachoendelea cha wiki mbili mimi na Mheshimiwa Mbunge tutapanga ratiba vizuri kwa sababu nadhani tukienda pamoja mimi na yeye tutafanya jambo ambalo ni la tija zaidi.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili Mheshimiwa Mbunge anasema hapo zamani eneo hili ni kweli lilikuwa linaonekana lina faida za kiuchumi na kijamii lakini kwa maoni yake anasema kwamba hali hiyo imebadilika kwa hivyo hivi sasa anadhani kwamba kuna haja ya Serikali kupitia upya mawazo au maamuzi hayo.
Mheshimiwa Spika, jibu ni kama lilivyo kwenye majibu ya msingi aya ya mwisho kabisa kwamba sasa Serikali tutakwenda kwanza kutoa ushauri lakini pia kushirikisha wataalam wa eneo hili ili tuweze kwa pamoja sasa kupima hicho ambacho tunasema kwamba zamani kilikuwepo lakini sasa hakipo. Mimi naamini tukienda wote tukakaa pamoja na kukagua maeneo yanayohusika tunaweza tukafikia muafaka. Ahsante sana.
MHE. PROF. NORMAN A. S. KING: Mheshimiwa Mwenyekiti, naogopa majibu kama haya yasije yakarudiwa mwakani. Kwanza, nini kauli ya Serikali kufanya commitment ya ujenzi hasa wa barabara hii? Kwa sababu nafahamu Hifadhi za Ngorongoro, Manyara na Serengeti zina sifa kubwa kwa sababu ya miundombinu kuwa imeboreshwa na hasa ya barabara.
Pili, sambamba na hilo, Pori la Mpanga Kipengere, mipaka imerekebishwa kiasi kwamba inaumiza Kata za Ikuo, Kigala, Mfumbi, hivyo kusumbua wananchi kiasi kwamba hakuna hata eneo la kujenga miundombinu. Nini kauli ya Serikali kuhusu hili? Kwa sababu upande wa TAMISEMI najua wameshalishughulikia. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Profesa Norman King juu ya uwepo wa uwezekano wa kurudiwa kwa jibu nililolitoa leo. Nia njema ya Serikali kwanza ni kuhakikisha kwamba Hifadhi ya Kitulo inaboresha au Serikali inaboresha utalii kwenye Hifadhi ya Kitulo, siyo kwa faida ya Kitulo peke yake na wananchi wa Kata tulizozitaja na Jimbo la Mheshimiwa Mbunge, lakini pia kwa ajili ya Taifa zima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi ya Kitulo tunaiboresha kwanza kwa kuboresha miundombinu ya ndani ambako tayari tumeboresha barabara za ndani na mageti ya kuingia ndani ya hifadhi, nyumba za wafanyakazi pamoja na ofisi. Pia tumeboresha upatikanaji wa bidhaa za utalii. Kwa sasa hivi hifadhi hii ni maarufu kwa ajili ya maua na hali ya miinuko (terrain) ya pale na hali ya hewa ambayo inafanana tu na nchi nyingine za Ulaya tofauti na hapa kwa maana ya baridi ya muda mrefu na vitu vya namna hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi tayari tunataka kurudisha wanyama ambao walikuwepo zamani lakini baadaye kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ujangili, wanyama hao wametoweka. Sasa tuna mpango wa kurudisha tena wanyama wakiwemo pundamilia, swala na nyumbu ili kuweza kuifanya hifadhi hii iweze kupanda hadhi, tuweze kupata watalii zaidi, ambayo itachangia kwa kiasi kikubwa kukuza utalii kwenye eneo la kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba ni nia ya Serikali na kwa kweli tumepania kuweza kupandisha hadhi ya utalii, siyo kwa Kitulo peke yake, bali kwa utalii wa eneo la Kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili; Mpanga Kipengere ni mojawapo ya maeneo ambayo tuna migogoro ya mipaka, lakini nataka kusema kwamba kama ilivyo kwa maeneo mengine kadhaa ambayo tumekwisha yaorodhesha, yanaendelea kushughulikiwa na Tume Maalum ya Serikali ambayo tumeiunda ya kushughulikia migogoro ya namna hii. Nafikiri tuwape muda mfupi tu ujao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati hii ilipata changamoto mbalimbali, mojawapo ikiwa ni ya kifedha, lakini sasa hivi tumetatua changamoto hiyo ya kifedha, wapo kazini na wanakwenda kwa kasi ili kuweza kutatua migogoro inayofanana na huu ambao uko pale Mpanga Kipengere.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ziada tu namwomba Mheshimiwa Mbunge, baada ya session hii nikutane naye ili niweze kupata details za status ya Mpanga Kipengere ili niweze kuwashauri wale ambao wanaendelea na kazi hii kwa maana ya Kamati ya Kitaifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wananchi waliokuwa na umri wa kuelewa mambo, mwaka 1956 Mwalimu Nyerere aliahidi ujenzi wa Bwawa la Stiegler‟s Gorge ili kuweza kutatua tatizo la umeme. Bwawa hili lingejengwa pale katika Kata ya Mwaseni. Ahadi hii ina miaka 61.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kufahamu kama ahadi hii ya Mheshimiwa Waziri aliyotuahidi hapa ujenzi wa mabwawa katika Kata za Mwaseni, Kipugira, Kilimani pamoja na Mkongo itachukua pia miaka 61 au itakuwa muda mfupi kidogo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Wizara ya Maliasili na Utalii inachangia pato la Taifa asilimia 19 na Rufiji yetu iko ndani ya hifadhi kwa zaidi ya nusu ya Rufiji, yaani square kilometer 6,500 ipo ndani ya hifadhi ya Maliasili na Utalii. Naomba kufahamu, mchakato wa ujenzi wa vyoo katika eneo la Selous pale Rufiji, leo hii watalii wanajisaidia katika maeneo ya hifadhi bila kuwa na vyoo. Naomba kufahamu, hili pato la Taifa mgawanyo wake ukoje katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii ili kuweza kusaidia wanyama hawa ambao wapo ndani ya hifadhi ikizingatia kwamba watalii wetu leo hii wanajisaidia sehemu ambazo ni za wazi bila kujisaidia eneo la vyoo.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza la wasiwasi au mashaka ya kwamba pengine hata ahadi hii tuliyoitoa hapa inaweza ikachukua muda mrefu ule alioutaja zaidi ya miaka 60 akifananisha na suala la mradi wa Stiegler‟s Gorge; kwanza nataka tu nimpe taarifa kwamba mradi wa Stiegler‟s Gorge akileta swali ambalo ni mahsusi kwa mujibu wa Kanuni za Bunge litajibiwa vizuri sana na Wizara ya Maji kwa sababu lina majibu sahihi kabisa na mahsusi ya kwa nini imechukua muda mrefu kiasi hicho kutekeleza mradi huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na majibu haya ya utekelezaji wa ujenzi wa mabwawa matano; kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kwamba hivi ninavyozungumza, kutokana na jitihada zake, wananchi wa Jimbo lake wanaelekea kupata majawabu ya changamoto kubwa hii ya kupata maeneo ya uvuvi hivi karibuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi karibuni kwa sababu ninavyozungumza sasa hivi tayari mawasiliano yameshafanyika kati ya Wizara yangu na Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji. Tumeshabadilishana uzoefu na taarifa na tayari tuna makisio ya awali ya gharama za ujenzi wa mabwawa hayo matano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kutokana na kiwango cha fedha kile ambacho tumekiona katika hatua za awali, tunafanya mapitio ili tujue ukubwa wa mabwawa yale lakini pia tujue namna ya kuyajenga ili kuweza kutumia gharama ambazo zitakuwa zina unafuu, lakini bado tufikie malengo ya kuweza kuwapatia mabwawa hayo wananchi.
Kwa hiyo, wananchi wa Rufiji wasiwe na wasiwasi, Mheshimiwa Mchengerwa anawapigania na watapata maeneo ya kuvua samaki mbadala nje ya Hifadhi ya Selous. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili; ni kweli utalii unachangia asilimia zaidi ya 17 katika pato la Taifa; lakini pia niongeze kwamba robo ya upatikanaji wa fedha za kigeni katika muda wa miaka mitatu mfululizo lilitokana na pato linalotokana na utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu changamoto aliyoisema ya eneo la maingilio ndani ya hifadhi, changamoto ambayo inaleta usumbufu kwa watalii, nataka kusema kwamba changamoto hii imeshamalizika kwa sababu tayari ni miongoni mwa mambo ambayo tumeyapa kipaumbele hivi karibuni, yale ambayo tunatakiwa kuyashughulikia kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua unapokuwa na changamoto kuna nyingine ni kubwa sana zinahitaji labda jitihada kubwa na rasilimali nyingi, lakini hizi nyingine ndogo ndogo kama hii, hizi ni quick wins, kwa hiyo, tunazifanyia utaratibu wa haraka. Nataka nimhakikishie kwamba kabla mwaka huu haujakwisha, tutakuwa tumetatua tatizo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. BONNAH M. KALUWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru
Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake. Kwa kuwa, Wizara ya Maliasili imelitelekeza
hili eneo kwa muda mrefu na hili eneo limekuwa ni eneo hatarishi na lipo katikati
ya makazi ya watu, watu wamekuwa wakipita hapo wanavamiwa na wengine
wameumizwa. Je, Wizara haioni sasa umefikia wakati muafaka kulirudisha hili
eneo Manispaa ya Ilala ili liweze kutumika kwa maendeleo ya Watanzania wote.
(Makofi)
Swali la pili; Jimbo la Segerea lina wakazi wengi lakini ndio Jimbo mpaka
sasa hivi halina kituo cha afya, halina soko, halina viwanda vidogovidogo
ambavyo wananchi au vijana wanaweza wakajiendeleza. Je, Wizara ya Maliasili
haioni kwamba umefika wakati ilirudishe hili eneo kwa wananchi wa Jimbo la
Segerea ili sisi tuweze kujenga kituo cha afya na mimi Mbunge wa Jimbo la Segerea nitatoa milioni 50 katika Mfuko wa Mbunge ili tuweze kuanzisha kujenga
kituo cha afya.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu
swali lake la kwanza Wizara haijatelekeza eneo la Msitu wa Kinyerezi na badala
yake miongoni mwa maeneo ambayo tayari yana maboya kwenye mipaka na
ambayo yana mabango na usimamizi wake unaendelea kwa kufuata mipaka
hiyo niliyoitaja ambayo imeshawekwa alama kama nilivyotangulia kusema eneo
la msitu huu ni mojawapo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema eneo hili ni la hekta 4.4 tu.
Eneo la hekta 4.4 ni dogo sana, tunapata changamoto kubwa sana kama Taifa
ya kwamba Miji inaonekana kama vile ili uone mahali kuna mji ni sawasawa
kwamba panatakiwa pawe mahali palipo wazi kabisa hapatakiwi kuwa na miti
hata kidogo. Hii ni dhana ambayo tunapaswa kuondokana nayo twende katika
mwelekeo ambao Miji yetu itakuwa pamoja na majengo na vitu vingine
unavyoweza kuviona kama miundombinu, misitu iwe ni sehemu mojawapo. Tuwe
na miti, bustani ndiyo tunaweza kuwa na miji ambayo itakuwa endelevu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili la mahitaji ya eneo;
nimesema kwenye swali la msingi, Ilala ina eneo kubwa bado kwa mujibu wa
sensa iliyopo ina jumla ya hekta 21,000. Kwa hiyo, hakuna uhaba wa ardhi, tuna
changamoto ya matumizi bora ya ardhi. Haya mambo mawili ni tofauti. Kukosa
ardhi au kuwa na uhaba wa ardhi na kukosa mbinu za matumizi bora ya ardhi ni
mambo mawili tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu narudia tena Mheshimiwa
Mbunge kwa kushirikiana na Baraza la Madiwani na Halmashauri ya Wilaya
inayohusika, waende wakakae wajaribu kuangalia Ilala kwa ukubwa wake na
eneo lake lote, miundombinu iliyopo na fursa zingine zilizopo za matumizi ya
ardhi, wafanye mpango bora wa matumizi ya ardhi ili waweze kupata maeneo
ya kuweza kujenga miundombinu aliyoizungumzia.
MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Wakati
likijibiwa swali juu ya Msitu wa Nyuki, Serikali imeeleza kwamba inakusudia
kuendeleza msitu huu kuwa sehemu ya vivutio vya utalii Dar es Salaam. Kwa
miaka mingi Serikali imekuwa ikitoa ahadi juu ya kuugeuza msitu wa akiba wa
Pande (Pande Forest Reserve) kuwa kivutio cha utalii, ikafikia hatua mpaka
Serikali ikatangaza tenda.
Sasa kama msitu huu mpaka leo haujakamilika kuwa kivutio cha utalii ni
miujiza gani ambayo Serikali inayo ili kuharakisha kwamba haya mapori ya Dar es
Salaam yageuzwe kuwa sehemu za utalii na kuingiza kipato kwa Dar es Salaam
badala ya kuyaacha kama yalivyo na hatimaye kugeuka kuwa misitu ya mauaji
kama ilivyokuwa pori la akiba la Mabwepande.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza
nimpongeze kwa mtazamo ambao ni chanya wa kwamba, kwanza
anakubaliana na dhana nzima ya matumizi bora ya maeneo ya misitu;
hapingani na dhana nzima ya Serikali kuhusiana na kuifanya misitu iwe ni
rasilimali ambayo inaweza kutumika kwa ajili ya maslahi ya jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kwamba kuna ucheleweshaji
kama ambavyo amesema; nataka nimtoe wasiwasi kwamba historia ni nzuri,
inatukumbusha tulipotoka, mahali tulipo na inatuwezesha kuona kule ambako
tunakwenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Mheshimiwa Mnyika akubaliane tu na
rai yangu kwamba tumetoka huko tulikotoka, mipango imekuwepo lakini sasa
awamu hii mipango hii ninayoizungumza ni uhakika na kwamba nataka anipe
muda wa mwaka mmoja tu, halafu aweze kuona katika eneo hili tunafanya nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa
kunipa nafasi. matatizo yaliyopo huko Segerea yapo pia katika Jimbo langu la
Manyoni Magharibi katika Halmashauri ya Itigi kuna msitu unaitwa Chaya Open
Area, ni kitalu cha uwindaji ambacho muda mrefu hakina Mwekezaji. Sasa
Serikali inataka kuondoa wananchi ambao wamekaa pale kwa ajili ya kulima na
wanafuga vizuri sana. Je, Serikali inaweza ikaona umuhimu wa wananchi wale
kuendelea kutumia Chaya Open Area ambapo ni eneo ambalo halina kabisa
faida kwa ajili ya uwindaji?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika,
anazungumzia eneo la Chaya na anatoa maoni kwamba pengine Serikali ilitoe
sasa eneo hili kwa ajili ya matumizi ya kibinadamu kwa wananchi wa eneo hilo
na wanaozunguka eneo hilo. Tumejibu swali hili mara nyingi kama Serikali
kwamba tunayo changamoto kama Taifa ya kwamba katika maeneo kadhaa
wananchi wamepata au wameonekana kuwa na uhitaji wa maeneo kwa ajili ya
matumizi ya kibinadamu yakiwemo makazi, kilimo pamoja na ufugaji. Kama
Serikali tumekwishasema kwamba jambo hili linatakiwa lishughulikiwe kisayansi na
kitaalam. Huwezi kuzungumzia juu ya uhaba wa ardhi juujuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wakati huu tunavyoendelea tayari Serikali
imekwishaunda Kamati ya Kitaifa inayohusisha Wizara nne ambayo inapita katika
maeneo yote ya nchi hii kuangalia kwa uhalisia kabisa wapi kweli kuna uhaba
wa ardhi na wapi kweli ardhi tungeweza kuitumia kwa namna bora zaidi. Kamati
hii itasaidia baadaye Serikali iweze kuja kusema kwamba eneo hili ni kweli
linaweza likabadilishwa matumizi na eneo lingine liendelee kubakia kutumika
kwa namna ambayo sote tutakubaliana tukiwa tunaongozwa na Serikali
kwamba matumizi hayo ya hivi sasa ni matumizi ambayo yana tija zaidi kwa
Taifa.
MHE. MARWA R. CHACHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, pengine Waziri wa Maliasili na Utalii au Waziri; katika Wilaya ya Serengeti ndani ya mbuga yetu ya wanyama ya Serengeti kuna mahoteli mengi na makampuni mengi ambayo kisheria wanatakiwa kulipa service levy, lakini kwa muda mrefu walikuwa mahakamani wakikataa na kupinga kulipa ushuru wa service levy. Sasa Serikali imewashinda, tumewashinda yale makampuni lakini mpaka sasa yale makampuni yanagoma kulipa ushuru wa service levy. Je, Wizara ya TAMISEMI na Wizara ya Maliasili na Utalii inaweza kutusaidiaje sisi Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti ili waweze kulipa arrears?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hapo siku za nyuma tumekuwa na hiyo changamoto ya hotels kutofuata utaratibu ambao tulikuwa tumeshauweka na kwa kweli ni kwa mujibu wa sheria kwamba, walipaswa kulipa zile kodi mbalimbali kwa utaratibu ambao Mheshimiwa Mbunge anauzungumzia lakini ni kweli suala hili lilifika mahakamani na hukumu ilitolewa na mahakama sasa kwa bahati mbaya utekelezaji wa hukumu haukuweza kuendelea kwa sababu tulikuwa na changamoto ya kutokuwa na bodi ambayo kwa mujibu wa sheria ndiyo inayopaswa kufanya maamuzi na kuchukua hatua. Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe taarifa kwa ujumla kwamba tayari bodi imekwishaundwa, Mheshimiwa Rais alishateua Mwenyekiti wa Bodi na bodi imekamilika iko tayari na kwamba hivi karibuni suala hilo litapatiwa ufumbuzi na majibu yatapatikana na bila shaka hakuna mashaka tutakwenda kutekeleza ile hukumu kama ilivyotolewa na mahakama.
MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu waliouliza swali hilo hilo la 0.3 percent service levy. Naomba kuuliza, je, Serikali itakuwa tayari pamoja na hiyo bodi mpya kuundwa, tunashukuru imeundwa kuwanyima leseni hoteli zote za kitalii ambazo zinafanya biashara ndani ya maeneo yetu ya halmashauri zote nchini ambao hawajalipa arrears za nyuma na kila mwaka kabla hawajapatiwa leseni mpya kama ilivyokuwa kwenye kodi nyingine, wasipewe leseni kabla ya kuhakikisha kwamba kodi zote za halmashauri zetu zimelipwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria na kila jambo ambalo ni kubwa linagusa maslahi ya wananchi, linagusa maslahi ya Taifa ni vizuri tukaliacha likaenda kwa kufuata taratibu za kisheria. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kuwa tumesema kwamba madamu bodi imeshaundwa, tunakwenda kupitia hukumu lakini pia kwa kuzingatia Sheria zilizopo tunaenda kuangalia namna ambavyo maslahi ya Taifa yanazingatiwa. Ikiwa kutakuwa kuna mapungufu kwenye Sheria basi tunaweza kulazimika kufanya maerekebisho ya Sheria lakini kama Sheria iko vizuri basi tutatekeleza Sheria jinsi inavyosema ili mradi tu mwisho wa siku maslahi na maslahi ya jamii yaweze kulindwa.
MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru na nashukuru pia kwa majibu kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa majibu ya
Mheshimiwa Waziri ni kwamba Serikali iko mbioni kufanya marekebisho ya sheria hii. Napenda kufahamu ni lini sasa Serikali itafanya marekebisho haya na kutenga eneo mahsusi
kwa ajili ya wakazi wanaoishi katika eneo hili la Bonde la Ngorongoro ili waweze kujihusisha na kilimo kwa sababu sio mazao yote yanayoharibu mazingira?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa
ukosefu wa maji kwa mifugo hususan msongamano ndani ya eneo dogo na kuharibu mazingira na kwa kuwa hifadhi hii bado ina maeneo ambayo yanaweza kutengwa kwa ajili
ya mifugo iweze kupata maji na Mheshimiwa Waziri Mkuu alishaiagiza Wizara hii kuhakikisha kwamba inatenga maeneo hayo ili wafugaji waweze kupata maeneo hayo kwa ajili ya
kunyweshea mifugo yao. Je, ni lini Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro itaweka maeneo haya maji na wananchi wanaoishi katika Bonde hili la Hifadhi ya Ngorongoro waweze kunywesha mifugo yao katika maeneo hayo na siyo kwenda kuharibu mazingira kama ambavyo sasa wanavyodaiwa
kufanya?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anataka kujua ni lini mabadiliko ya sheria kama ambavyo tumejibu katika swali la msingi yanafanyika? Mchakato wa mabadiliko ya sheria
unatanguliwa na shughuli kadhaa za kitaalam ambapo kutokana na shughuli hizo za kitaalam ndipo mapendekezo ya mabadiliko ya sheria yanapelekwa katika hatua mbalimbali za Serikali ili hatimaye mabadiliko ya sheria yale yaweze kuwa na tija kwa sababu yatakuwa yana-input ya kitalaam.
Mheshimiwa Spika, hivi ninavyozungumza, katika
kipindi cha wiki moja kikosi maalum cha watu wanaotakiwa kufanya sensa kama jambo la kwanza kabisa la kulifanya ili kujua ukweli wa hali halisi ya Ngorongoro kitaanza kazi. Kazi ambayo itafanyika kwa muda wiki moja. Hii inatokana na ukweli kwamba mwaka 1959 wakati Ngorongoro inatengwa kama eneo la hifadhi kulikuwa na jumla ya wakazi 8000 ndani ya eneo lile. Kufikia mwaka 2013 tayari kulikuwa na wakazi jumla ya 87,851, hii ni takribani wastani wa ongezeko la wakazi 1500 kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, changamoto hii ni
kubwa na hivyo hata mabadiliko ya sheria yanatakiwayaangalie uhalisia ambao utakuwa ni uhalisia wa kisayansi. Kwa hiyo, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, ndani ya kipindi cha mwaka wa fedha ujao tutakuwa tumeanza na kukamilisha utaratibu wa mabadiliko ya sheria
inayohusika.
Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili
anazungumzia juu ya suala la ukosefu wa maji na ambalo lina maagizo mahsusi kutoka kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ni kweli, kulikuwa na maagizo ambayo yalikuwa yanataka kutatua changamoto ya maji katika kipindi cha mpito wakati ambapo tunasubiri mabadiliko yale ya sheria ambayo yataweka misingi ambayo itakuwa ni ya kudumu.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mpito suala la maji kwa ajili ya mifugo linashughulikiwa kwa kujenga mabwawa katika maeneo ambayo yanaonekana kwamba uwepo wa mabwawa katika maeneo hayo utatatua changamoto ya mahitaji ya maji kwa mifugo. Mamlaka ya
Hifadhi ya Ngorongoro imetenga fedha katika bajeti hii na Waheshimiwa Wabunge mkiipitisha, basi tunaweza kutatua tatizo hili kwa namna ambayo itakuwa ni toshelezi. Kwa hiyo,
namuomba Mheshimiwa Mbunge afanye subira, asubiri Bajeti ya Serikali, bajeti ya Wizara hii itakapopita, hasa kwa upande ule wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro tutakuwa tumeweza kuweka tengeo la kuweza kutekeleza agizo
la Mheshimiwa Waziri Mkuu ipasavyo.
MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuuliza swali moja tu la nyongeza. Tatizo la Hifadhi ya Ngorongoro linafanana sana na lile tatizo la Hifadhi ya Swagaswaga ambalo linaunganisha Wilaya za Kondoa na Chemba. Kumekuwa
na matatizo watu wengi wamezuiwa kulima na
nilishakwenda mimi na Mheshimiwa Naibu Waziri katika eneo hilo na akatoa maagizo kwamba, ufanyike utaratibu wa kuweka mipaka upya, lakini jambo hili halijafanyika hadi sasa. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuweka mipaka ili
wananchi wa Lahoda, Kisande, Iyoli pamoja na Handa waweze kuondokana na tatizo hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii. Ni kweli nilifanya ziara katika eneo hili ambalo linahusika na hifadhi yetu ya Swagaswaga na niliambata na Mheshimiwa Mbunge na ni kweli niliacha maagizo kama anavyosema. Pia siyo tu agizo, tuliendelea na utaratibu ule wa kuunda kikosi kazi ambacho kilihusisha Wizara nne na ambacho kimekuwa kikiendelea na kazi yake
kwa muda wa miezi michache iliyopita. Sasa hivi kamati ile imeshaandaa mapendekezo ya awali ambayo yamekabidhiwa tayari kwa Kamati ya Makatibu Wakuu, baada ya pale yanaenda kukabidhiwa kwa Baraza la Mawaziri, baadaye kwenye ngazi za juu, ili tuweze kupata
mwelekeo zaidi wa kwamba nini kifanyike ili kuweza kukamilisha utaratibu wa kuweka mipaka.
Mheshimiwa Spika, lakini kwa maana ya maeneo yale ambayo hayana migogoro kabisa, suala la uwekaji wa mipaka limekuwa likiendelea na hifadhi kadhaa tayari zimeshakamilisha utaratibu huo. Mheshimiwa Mbunge akiniona baada ya hapa tutaweza kuangalia kwenye orodha kama eneo lake limepangiwa lini kukamilisha utaratibu wa
kuweza kuweka mipaka.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro wamekuwa wakikumbwa na changamoto kubwa sana kwa sababu wanaishi katika eneo la hifadhi. Hata hivyo kumekuwa na ahadi nyingi za Serikali
za kumaliza hiyo changamoto lakini hakuna mafanikio na mpaka leo wananchi wale wanaishi tu kwa matumaini. Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba wamekataza mifugo isiingie crater lakini kuna changamoto ya upatikanaji wa maji. Kumeshawahi kutengwa takribani shilingi bilioni tano na zimetumika, wamejenga ranchi kwa ajili ya kuhifadhi mifugo isiingie crater na haitumiki. Je, ni kwa nini ranchi imejengwa kwa gharama kubwa halafu haitumiki mpaka sasa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, changamoto za Hifadhi ya Ngorongoro ni kubwa na nyingi. Hata hivyo, napenda ieleweke kwamba katika kusimamia uhifadhi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro jambo hili sisi wote kwa pamoja tunatakiwa tuzingatie ukweli kwamba maslahi ya mtu mmoja mmoja yatazingatiwa, maslahi ya makundi yatazingatiwa lakini mwisho wa siku maslahi ya Taifa yanayotokana na kuhifadhi eneo lile ndiyo
yatakayopewa kipaumbele.
Mheshimiwa Spika, ni kweli, hapa na pale katika
kipindi chote cha uwepo wa sheria hii tunayoizungumzia ya mwaka 1959 mengi yametokea. Yako yale ambayo Serikali ilisema itatekeleza, tumetekeleza kikamilifu, yako yale ambayo bado Serikali inaendelea kuyatekeleza, lakini tumesema msingi wa kuweza kushughulikia tatizo hili vizuri na kikamilifu ni kufanya marekebisho ya sheria. Kwa sababu kufanya kitu chochote kile nje ya sheria kwa ajili tu ya kutaka
kujibu hoja za makundi au za mtu mmoja mmoja ni jambo ambalo halitaweza kutufanya tukafanikiwa.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashauri Mheshimiwa Mbunge na wadau wengine wote na Taifa kwa ujumla tufanye subira. Tusubiri mabadiliko ya sheria ambayo yataweka misingi sasa ya kuweza kutatua changamoto hizi
kwa namna ambayo itakuwa ni endelevu.
MHE. MUSUKUMA J. KASHEKU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nilitaka tu kumwambia kwamba, yale aliyoyajibu hapa si sawa na uhalisia ulioko kule Jimboni.
Wananchi wangu wa vijiji vya Bugurula, Kasota, Nyawirimila, Sungusila na Kakubiro, wamewekewa matangazo mwezi mmoja uliopita na wakapelekewa barua za kuondoka kwenye vijiji ambavyo tayari vina shule na sasa Waziri anasema wao hawakuwa na huo mpango na hawajafanya wanaendelea na utaratibu na wameweka vigingi. Nilikuwa nataka kujua Waziri kama hizi taarifa alizozitoa ni sahihi ili niwaambie wale wananchi wangu kule wayang’oe yale matangazo yaliyowekwa kule? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kutokana na mkanganyiko wa mipaka ya vijiji na mapori ya hifadhi kumesababisha mpaka tunavyozungumza sasa kuna operesheni zinafanyika kwenye Mkoa wa Geita na Mkoa wa Biharamulo, Serikali ilitoa tangazo la siku tatu wananchi waondoe mifugo iliyopo kwenye hifadhi; siku tatu ng’ombe zitoke kwenye eneo la hifadhi kana kwamba hizi ng’ombe sijui zina mota miguuni, lakini wananchi wa Kisukuma hawakuwa na tatizo walitii amri bila shuruti.
Na kwa kuwa waliopo kule wahifadhi wameidanganya Serikali kwa kuwaambia kuna mifugo milioni 60 na kule hakuna mifugo milioni 60; wamezikosa baada ya kupewa hiyo bajeti ya operesheni wakaikosa mifugo wananza kukamata sasa kilometa saba kwenye vijiji na wakati kuna beacon zinazoonesha mipaka ya kijiji. Je, Waziri
husika anatoa kauli gani kwa wananchi ambao
wamekamatiwa ng’ombe zao Ngara, Katente na Chato walioko mahakamani na wameshapewa hukumu ya ng’ombe zao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii na kwa hiyo kwa kiasi kikubwa anafahamu uzito, upana na ukubwa wa changamoto inayohusiana na suala la uhifadhi na
muingiliano wa shughuli za kibinadamu katika maeneo mbalimbali nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii ni kubwa na haifanani kutoka mahali pamoja hata mahali pengine. Yapo matatizo yanayohusiana na wakulima na yapo matatizo yanayohusiana na wafugaji. Katika swali lake la msingi Mheshimiwa Mbunge alizungumzia juu ya suala la maeneo ya vijiji ambayo yamo ndani ya hifadhi ya Geita na kweli lilikuwa ni suala la mipaka baina ya vijiji na maeneo hayo husika. Na kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi ni kwamba Wizara yangu kwa niaba
ya Serikali haijafanya operesheni yoyote ya kuondoa wanavijiji katika maeneo hayo. Lakini nimesikia alivyosema kwamba kuna matangazo yamebandikwa huko ambayo sisi kama Wizara hata ninaposimama wakati huu mahali hapa
bado hatuwezi kuthibitisha uwepo wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya hapa kwa kuwa Serikali ni pana iko mamlaka ya Wilaya, Mkoa na ipo Serikali Kuu kupitia Wizara, sote sisi ni Serikali. Baada ya hapa nikutane naye ili tuweze kufuatilia matangazo hayo juu ya uwepo wake na
uhalali wake ili tuweze kujua namna ya kuweza kushughulikia tatizo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu swali lake la wale wafugaji na mifugo katika maeneo ya Geita, Biharamulo na maeneo mengine ambapo zipo operesheni zinaendelea sasa hivi zikiendeshwa na mamlaka za Mikoa na Wilaya huko zilipo, kama nilivyotoa maelezo katika jibu langu la msingi, migogoro ipo katika maeneo mengi, lakini kila mahali, kila mgogoro ni wa aina yake; chanzo tofauti, ukubwa tofauti na kwa hiyo tarajia kwamba utatuzi wake pia utakuwa upo
tofauti. Katika maeneo aliyoyataja uingiaji wa mifugo katika maeneo yaliyohifadhiwa ni mkubwa sana tena uliopelekea hata kuingia kwa mifugo kutoka nchi jirani na yeye amesema.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Serikali kupitia
Mamlaka ya Mkoa imeendelea kufanya operesheni hizo kwa sababu kimsingi hatua za Serikali tulizotangaza kwamba zinaendelea kuchukuliwa haziwezi kukamilika leo au kesho
kwa sababu zinafuata taratibu za kushughulikia changamoto za Kiserikali ambazo aghalabu huchukua muda mrefu. Katika kipindi hicho tukiacha ng’ombe waendelee kubaki katika
maeneo hayo ya hifadhi, wakati utakapofika
tumekwishapata ufumbuzi wa nini kifanyike hifadhi hizo hazitakuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe
Mheshimiwa Mbunge utaratibu ambao unaendelea hivi sasa wa Serikali wa kushughulikia changamoto hizo kwa uzito wake na katika maeneo ambayo athari ni kubwa huo utakuwa ni
utaratibu wa Serikali na aendelee kuunga mkono jitihada za Serikali za kuamua kusimamia uhifadhi kwa maslahi ya nchi yetu hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kutakuwa na jambo lingine ambalo ni mahususi kuhusiana na hatua hizo ambazo Serikali inachukua katika ngazi hizo za Mikoa na Wilaya basi anaweza kulileta, nimesema yeye ni Mjumbe wa Kamati
inayosimamia maliasili kwahiyo tunaweza kupokea maoni yake juu ya namna bora zaidi ya kuweza kushughulikia tatizo hili lakini kwa mujibu wa sheria. Katika hili sheria, kanuni na taratibu zitazingatiwa katika kushughulikia changamoto hizi.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa nitoe majibu ya ziada pamoja na majibu mazuri ambayo yametolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la msitu katika Wilaya na eneo lilozunguka Mji wa Geita limefikishwa pia kwenye Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Geita na maazimio yaliyofikishwa yameletwa kwetu kwa ajili ya kufikiria ni namna
gani katika maeneo ambayo watu wanaishi tunaweza kupunguza eneo la msitu kwa ajili ya matumizi mengine ili kukidhi hali halisi ya Mji Mkuu wa Mkoa ambao sasa uko pale Geita.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, jambo hili
tunaendelea kulizungumza na Mheshimiwa Mbunge awe na subira wakati Serikali ya Mkoa na Wilaya inapoongea na Wizara kuhusu msitu huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili; wapo ng’ombe ambao ni wengi sana katika maeneo ya misitu ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja. Mifugo hii ipo kwenye maeneo ya hifadhi kinyume cha sheria zetu; kinyume cha Sheria ya Uhifadhi wa Misitu Na. 5 ya mwaka 2009 kifungu cha 21(1). Na wananchi hawa wanajua kwamba wapo kwenye Hifadhi za Taifa kinyume cha sheria; walipewa muda wa kuondoka na tangazo la Mkoa na muda ule ukamalizika. Huwezi kusema mtu ambaye anafanya makosa ya kisheria kwamba hakupewa muda wa kutosha wa kufanya makosa yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitumie nafasi hii kuwashauri wafugaji wote ambao wana mifugo yao ndani ya maeneo ya Hifadhi za Taifa kinyume cha sheria zetu kwamba watoe mifugo hiyo mapema iwezekanavyo kabla Serikali haijachukua hatua ya kisheria kudhibiti mifugo hiyo.
MHE. JOHN H. WEGESA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa mara nyingine kwa kuniona na kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza kwa niaba ya watu wa Tarime.
Mheshimiwa Naibu Spika, GN hizi zilizotangaza haya maeneo na kuweka mipaka ya mapori ni ya miaka 1984; vijiji vingi ni vya miaka ya 1970, 1975 na kuendelea. Kwa hiyo, GN hizi zimetangazwa vijiji vikiwepo ukichukua Kata kwa mfano ya Kwihancha, Goronga na Nyanungu vimepakana na Pori la Serengeti; vijiji vyote vya maeneo haya ni vya miaka ya 1970 na vimesajiliwa vina usajili. Lakini watu wa Serikali wameanza kuhamisha kwa kutumia GN miaka ya 1990 mpaka sasa hivi wanazidi kurudisha watu nyuma, watu hawana maeneo ya kulima wala ya kuchungia.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Waziri watatue hili tatizo kwa haraka ili watu waendelee kuishi maisha yao ya kawaida na wasiendelee kuona wafugaji kwamba ni wahaini katika nchi yao, wawaruhusu ng’ombe wao waendelee kuchunga kwenye maeneo ambayo ni ya vijiji vyao kihalali na kisheria.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ulivyosema kwa kiwango kikubwa yale yalikuwa ni maoni au ushauri lakini ni vyema sauti ya Serikali ikasikika na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kufanya marekebisho madogo tu kwamba sio vyema kujumuisha au kutoa kauli ya jumla kwamba GN zote ni za miaka 1980. Nadhani katika eneo mahususi analolitaja inawezekana ipo hivyo lakini utaratibu ambao utaweza kutufikisha mahali ambapo patakuwa ndio pana usahihi zaidi ni kwa kuchambua kila kesi kwa kesi na kila hoja kwa hoja kwamba eneo fulani linahusishwa na GN namba fulani,
tutakwenda kuiangalia kwamba ni ya mwaka gani ili tuweze kujua eneo lililohifadhiwa na kijiji kilichopo kipi kilitangulia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hata hivyo kutangulia au kuja baadae pengine inaweza kuwa sio hoja ya msingi sana; hoja ya msingi itakuwa ni uhifadhi kwa maslahi ya Taifa. Na hivyo ndio maana tumesema kwamba tunayo tume
ambayo inaendelea kufanya kazi ambayo itahusisha pia na kufanya mapitio ya hayo yote tunayoyazungumzia. Kamati ambayo nimesema jana wakati najibu swali, lakini narudia tena leo ipo katika hatua ya kupitiwa na Makatibu Wakuu
na baada ya pale itakwenda kwenye hatua ya Mawaziri halafu baadae kwenye ngazi za mamlaka za juu za Serikali.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa tatizo lililopo katika misitu ya Geita linafanana sana na tatizo lililopo katika Msitu wa Shume ambapo katika vijiji vya Shume, Nywelo na Mkuhnyi ambavyo vipo katika Kata ya Manolo navyo eneo la Msitu wa Hifadhi wa Shume umeingia katika maeneo ya vijiji ambako wananchi mara nyingi ndiko wanakofanya shughuli zao za kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, na tatizo la mgogoro huu pia limeripotiwa katika Randama ya Wizara ya Ardhi. Je, ni lini sasa Serikali itakaa na wananchi hawa wa vijiji vya Shume, Nywelo pamoja na Mkunki ili angalau waweze kutatua tatizo hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, tumesikia, tumepokea shamba la msitu wa kupandwa wa Shume uliopo katika maeneo yale ya vijiji alivyovitaja vya Shume, Nywelo na Mkunki. Ni suala ambalo kama alivyosema mwenyewe limeorodheshwa kwenye
orodha ya maeneo ambayo yanatakiwa kushughulikiwa chini ya orodha ya migogoro ya ardhi iliyoandaliwa na Wizara ya Ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana kwa
kutukumbusha licha ya kwamba lipo kwenye orodha na kwa kweli kwa namna ambavyo anaweza kuwasemea wananchi ya maeneo haya kama mwakilishi wao na nimuahidi sambamba na kazi inayoenda kufanyika chini ya kamati iliyoundwa; mimi na yeye tutapanga tutaweza kwenda kwenye hili eneo tukaangalie uhalisia ili tuweze hata kuishaurihiyo kamati.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kuna tatizo pia la mipaka kati ya TFS na vijiji Wilayani Kondoa; vijiji vya Mnenia, Masanga, Itolowe na Kasese ambapo beacon za TFS zimeingilia katika mashamba ya wanavijiji hawa. Sasa ningependa kujua Serikali ina mkakati gani au ni lini itarekebisha tatizo hili ambalo linawaacha wanavijiji hawa njia panda? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikia akisema kwamba katika vijiji alivyovitaja beacons za TFS kwa kauli yake zimeingia katika mashamba ya wananchi kwenye vijiji hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena kwamba hii
ndio sababu tumeunda kamati maalum kwa sababu kusema tu moja kwa moja kwamba beacons zimeingia kwenye maeneo ya mashamba ya watu bila kuangalia kwamba upo
uwezekano mashamba ya watu yameingia ndani ya maeneo ya hifadhi haitakuwa sahihi katika hatua hii. Kwa hiyo, tuipe nafasi Serikali iweze kuendelea kufanya kazi ya kwenda kufanya utafiti wa kwenye site wa kuangalia uhalisia ulivyo tukipima kwamba ni kipi kimeingia upande upi lakini wakati huo huo tukiangalia zaidi maslahi ya hifadhi ambayo ndio priority kwa Taifa.
MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana; lipo tatizo kubwa kati ya Uwanda Game Reserve na vijiji vya Kilangawana, Maleza, Legeza, Mpande, Ilambo, Mkusi, Iweliamvula na Ngomeni. Kwa watu wa TFS
kuhamisha mipaka inayotambulika toka enzi za nyuma na kusogeza katikati ya vijiji. Tatizo hili ni kubwa sana na mimi nilishaenda mara kadhaa kumwambia Waziri kwamba naomba afike asikilize pande zote mbili kwa sababu ninachokiona hawa askari wa TFS ni kama wanagandamiza wananchi wakati jambo lipo wazi. Je, ni lini Serikali itatuma uongozi wa kwenda kuangalia haki juu ya wananchi wale?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, anazungumzia juu ya suala la Uwanda Game Reserve na ujirani wake na vijiji vilivyopo jirani na eneo hili la hifadhi. Na hoja yake inafanana na zile hoja zilizotangulia
pale mbele kwamba mipaka iliyowekwa na TFS katika miaka ya karibuni au katika siku za karibuni imeingia ndani ya maeneo ya vijiji.
Kama nilivyosema hapo awali kwamba sio vema
kwenda moja kwa moja na kutoa kauli ambayo inaonekana kama ni ya uthibitisho au ni ya ukweli kwamba mipaka ya hifadhi ndiyo iliyoingia kwenye maeneo ya vijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niweze kusema jambo moja tu hapa kwamba tuelewane kitu kimoja kwamba mipaka tunayoizungumzia ya miaka mingi haikuwa na alama; kwa hiyo, kuna suala la kuweka mpaka kuwepo lakini kuna suala pia la mpaka kuwekewa alama.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika miaka ya karibuni kilichofanyika au kinachoendelea kufanyika ni kuweka alama za kudumu hizo beacons au maboya au unaweza kutafuta
lugha nyingine yoyote ya Kiswahili, lakini ni alama
zinazoonekana. Sasa wakati wa kuweka alama
zinazoonekana Serikali inafuata mipaka ambayo ipo kwa mujibu wa maandishi kwa kutumia GPS coordinates kwenye ramani ambayo haikuwa imewekewa alama. Sasa kwa kuwa wananchi hawakuiona ile mipaka kwa alama zinazoonekana
licha ya kwamba kwa mujibu wa sheria zipo kwenye ramani, sasa hivi wananchi wanadhani kwamba alama hizo zimehama.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba alama hizo zinawekwa mahali pale ambapo ndipo kwa mujibu wa sheria alama hizo ndipo zilipo na kwa hiyo sasa ni vema tukasubiri utaratibu unaofanyika na Serikali wa kwenda kuweka alama kwenye maeneo hayo kwa sabau kuweka alama sio maana yake tayari hatua za mwisho zimeshafanyika za kuweza kuwahamisha wananchi; tunaweka kwanza alama kutambua maeneo hayo halafu baada ya pale tunaweza kuendelea na kuelimishana kwamba kwa nini mpaka upo hapa na sio pale.
MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, ni kwa nini Serikali inaruhusu na kutoa vibali kujengwa kwa hoteli za kitalii kuzunguka rim ya Ngorongoro Crater hali inayoharibu mandhari ya Ngorongoro lakini pia ni vyanzo vya maji kwa ajili ya hifadhi hii?
Swali la pili, wakati Ngorongoro inaanzishwa mwaka 1959 ilikuwa na wakazi 8,000 lakini kwa takwimu za mwaka 2013 hifadhi hii ina wakazi elfu 87.7 kwa hivyo leo tunavyozungumza ni zaidi ya laki moja. Lakini kuongezeka kwa watu maana yake ni kuongezeka kwa mifugo lakini pia kuongezeka kwa mahitaji na huduma mbalimbali.
Naomba Serikali iliambie Bunge, wakati Hifadhi
inaanzishwa, master plan ya Ngorongoro Crater inasemaje juu ya uwepo wa idadi gani ya watu ambao wanaweza kuhudumiwa kikamilifu wakapata huduma zote, lakini pia hadhi ya hifadhi ikaendelea kubaki kama ambavyo tunategemea? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumpongeza Mheshimiwa Magdalena Sakaya kwa kuwa kwanza yeye ni Mhifadhi kitaaluma lakini pia amekuwa miongoni mwa Wajumbe wa
Kamati ya Maliasili na Utalii ambao wamekuwa katika mstari wa mbele kuishauri Serikali kuhusiana na masuala ya maliasili na utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza ni kweli ukienda Ngorongoro leo utakuta kuna hoteli zimejengwa kandokando ya crater kwenye eneo linaloitwa rim ya crater. Lakini uwepo wa hoteli hizi ni ambao umetokana na mabadiliko mbalimbali tangu sheria ilipokuwa imeandikwa kwa mara ya kwanza mwaka 1952.
Sheria hii ilifanyiwa marekebisho ya kwanza mwaka 1963 lakini baadae sheria hiyo ilifanyiwa marejeo mwaka 2002. Katika vipindi hivyo mabadiliko mbalimbali yametokea, sasa tangu
amri ilivyotolewa kutokana na sheria kwamba sasa hakuna kuanzisha hoteli kandokando ya crater na hasa kwenye eneo la rim hakuna hoteli nyingine yoyote imeanzishwa katika kipindi hicho. Nyingi zilizopo ni zile ambazo zilianzishwa katika
kipindi cha nyuma.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la pili ni kweli kwamba mwaka 1959 wakati sheria hii inapitishwa kulikuwa na takribani watu 8,000 katika eneo la hifadhi na kwamba ni ukweli ulio wazi takwimu zinaonesha mwaka 2013 tayari idadi ya watu ilifikia 87,851. Ukifanya hesabu ni kama vile ongezeko la wakaazi 1500 takriban kwa kila mwaka. Hili ni ongezeko linaloashiria kwamba leo tukifanya takwimu kweli tunaweza kupata wakaazi wanaokaribia laki moja, hii ni idadi kubwa sana na ni tishio kwa shughuli za hifadhi katika eneo hili la Hifadhi la Ngorongoro.
Mheshimiwa Spika, hatua ambazo Serikali inafanya kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni uwepo wa sheria peke yake utakaoweza kutoa mwongozo na mwelekeo namna gani tunaweza kukabiliana na changamoto za hifadhi katika eneo la Ngorongoro. Sasa sheria iliyopo ina mapungufu ni kweli na ndiyo maana nimesema katika jibu la msingi kwamba katika kipindi cha muda mfupi ujao mchakato wa kufanya marekebisho ya sheria ili iendane na matakwa ya sasa ya uhifadhi katika eneo linalohusika utaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge, mara Serikali itakapoleta sheria hii mbele ya Bunge hili baada ya kukamilisha michakato ya awali, wote tuwe na spirit ya kutaka uhifadhi uimarishwe katika eneo la
Ngorongoro ili tuweze kupata faida zote za urithi na kiuchumi na faida nyingine zote zinazotokana na uhifadhi kupitia utalii.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika,
ahsante kwa nafasi hii.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hadhi ya Hifadhi ya
Ngorongoro inafanana kabisa na hadhi ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro, mlima ambao ni mrefu sana, mlima ambao unaingiza kipato kikubwa kwenye utalii, mlima ambao ni wa pekee wenye theluji katika nchi za tropic.
Je, Serikali sasa ina mpango gani kuhakikisha
kwamba wanaozunguka mlima ule wanaweza kuwekwa katika hali ambayo wataendelea kuutunza ili ile theluji isije ikayeyuka yote na ule mlima ukabakia katika ubora wake?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza ni kweli kwa maana ya sifa za uhifadhi, lakini pia faida za kiuchumi zile za Ngorongoro zinafanana kwa karibu sana na za hifadhi ya Mlima Kilimanjaro. Sasa kuhusu swali lake nini Serikali itafanya ili kuweza kuboresha zaidi shughuli za uhifadhi kwa faida za kiuchumi Kitaifa lakini pia kwa faida ya jamii inayoishi kwenye maeneo haya ya Hifadhi ya Kilimanjaro.
Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba kwanza Serikali inatambua umuhimu wa ushiriki wa wananchi katika shughuli za uhifadhi na kwa kweli tunatoa wito kwa wananchi wanaoishi katika eneo hili la Mlima Kilimanjaro waweze kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha kwamba uhifadhi unaimarishwa katika eneo la Kilimanjaro. Mheshimiwa Spika, jitihada za Serikali ni kuendelea kusimamia sheria iliyopo lakini pia tunakaribisha maoni kutoka kwa wananchi wanaoishi kwenye eneo hilo hata wengine waweze kutusaidia ili kuweza kupata maoni ya
wananchi yatakayotuwezesha kuboresha zaidi shughuli za uhifadhi katika eneo la Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu yasiyoridhisha ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa katika jibu la msingi Mheshimiwa Naibu
Waziri amesema wafanyakazi hao wa Seventy Seven walilipwa, siyo kweli walilipwa awamu ya kwanza, awamu ya pili haikuwafikia wafanyakazi hawa na baada ya malalamiko Wizara ilituma wakaguzi mwaka 2003 wakakagua wakajua kuna tatizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa watu hao wamekuwa wakihangaika muda mrefu kutafuta haki zao waliandika barua Ofisi ya Rais, tarehe 17 Machi, 2016 walijibiwa barua kutoka Ofisi ya Rais ikienda kwa Waziri wa Maliasili kuwa ashughulikie tatizo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, vilevile walilalamika Ofisi ya Waziri Mkuu na kuna barua ilikuja ya tarehe 4 Novemba, 2016 kuwa tatizo hili lishughulikiwe.
Je, Serikali haioni kwamba wanyonge hawa wanapoteza muda mwingi wakitafuta haki yao huku yenyewe ikidai imewalipa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wa Maliasili alishapewa agizo kutoka Ofisi ya Rais ashughulikie, ni kwa nini wanasuasua wananchi wakiendelea kupata taabu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni swali la nyongeza ambalo limejitokeza na hoja ambayo nimeisikia kwa mara ya kwanza hapa, basi nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge anipe fursa katika kipindi cha mapumziko leo hii nilifanyie kazi halafu nimpe majibu ambayo yatakuwa ni ya uhakika zaidi.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sekunde moja naomba niendelee kutoa pole kwa wananchi wangu wa Rufiji hususan tukio la jana ambapo Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyambuju alitaka kuuawa lakini alisalimika baada ya kukimbia kugundua majambazi wale wameshaingia nyumbani kwake,
taarifa ambazo nimezipokea muda huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili tu ya nyongeza; la kwanza nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri migogoro baina ya wananchi na wahifadhi imechangiwa na kuondolewa kwa mipaka ya awali iliyokuwepo hususan katika Kata ya Mwaseni na wananchi kuzuiliwa kuvua samaki
wale ambao wapo katika vijiji vinavyopakana na hifadhi. Naomba kufahamu Serikali ina mpango gani sasa ili yale mabwawa matano niliyoyaomba kwenye Wizara ya Maliasili na Utalii yaweze kuchimbwa haraka katika Kata ya Mwaseni, Kata ya Kipugira hususan maeneo ya Nyaminywili, Kipo na Kipugila pia katika Kata ya Ngorongo? Naomba kufahamu Serikali inaharakisha vipi
mchakato wa uchimbwaji wa mabwawa ya samaki kwa wananchi wangu wa maeneo hayo?
Mheshimiwa naibu Spika, lakini pili……
Mheshimiwa Naibu Spika, ninafuta hilo swali la samaki, naomba la mgogoro wa mipaka libaki. Swali la pili, watumishi wa hifadhi wamekuwa
wakiweka beacons na alama kadhaa katika baadhi ya nyumba hususani katika maeneo ya Kipugila maeneo ya Nyaminywili na maeneo mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato wa uwekaji wa beacons unakiuka Ibara ya 13 ya Katiba, pia unakiuka Ibara ya 16 ya Katiba ambayo inazungumzia haki za msingi za wananchi ubinafsi wao, ufamilia wao pamoja na uhifadhi wa maskani zao. Ninaomba kufahamu je, Wizara hii ya Maliasili na Utalii imedhamiria kabisa kukiuka Katiba ya haki za msingi ya Ibara ya 13 na Ibara ya 16, katika kuweka beacons na kusababisha uhuru wa wananchi wa mnaeneo husika kukosa haki zao za msingi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuanza na swali lake la pili. Uchukuaji wa hatua wa wawekaji mipaka kwenye maeneo yote ya hifadhi unafanyika hivyo kwa mujibu wa sheria. Kama tunavyofahamu zimetungwa na Bunge lako Tukufu jambo ambalo limefanyika pia kwa mujibu wa Katiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ule ni utekelezaji wa sheria ambazo zipo kwa mujibu wa Katiba, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba hata mara moja Serikali kupitia Wizara ya Maliasili haiwezi kuvunja Katiba. Iwapo kuna jambo lolote mahususi ambalo anadhani kwamba linaweza kufanana na hicho anachokisema basi namkaribisha aweze kuja kuniona tuweze kulijadili na kuweza kulipatia ufumbuzi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili ambalo lilikuwa la kwanza la uwekaji wa mipaka au uwekaji wa alama. Uwekaji wa alama ni hatua inayochukuliwa baada ya kuwa tayari mipaka ilikuwepo miaka mingi iliyopita. Wakati wa utekelezaji wa zoezi la uwekaji wa alama Wizara
inafanya mazoezi haya kwa kushirikisha wananchi katika maeneo yanayohusika.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini katika maeneo
ambayo ameyataja Mheshimiwa Mchengerwa zoezi hili limefanyika kwa utaratibu huo wa kushirikisha wananchi, iwapo kuna hoja mahsusi zinazohusiana na alama hizo basi anaweza kuzileta kwa kutaja vijiji vyenyewe hasa ili tuweze
kuona namna ambavyo tunaweza kwenda kuona namna bora zaidi ya kwenda kuweka alama hizo. Nisisitize kwamba zoezi hili kwamba zoezi hili ni agizo la Serikali kupitia maagizo ya Viongozi Wakuu wa Serikali akiwemo Mheshimiwa Waziri
Mkuu na kwa hiyo litaendelea lakini jambo la msingi tutaendelea kushirikisha wananchi ili liweze kuwa zoezi rafiki.
MHE. JOSHUA S. NASSARI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona na mimi niulize swali moja dogo la nyongeza. Migogoro ambayo imeendelea kuwepo baina ya vijiji ambavyo vinazunguka hifadhi haviko kwa Mheshimiwa Mchengerwa peke yake, pale Arumeru kuna Hifadhi ya Taifa ya Arusha (Arusha National Park) na imekuwa na mgogoro wa siku nyingi sana hususani kijiji cha Momela, kitongoji cha Momela na hifadhi. Hifadhi ya Taifa ya Arusha ni miongoni
mwa hifadhi changa ambazo zimekuja kuanzishwa miaka ya juzi juzi tu.
Swali langu kwa Mheshimiwa Waziri Makani ni kwamba ni lini basi atakuwa tayari tuende Arumeru ili tuweze kwenda kuhuisha mgogoro
ambao umekuwepo baina ya Kijiji cha Momela wananchi wa King’ori na wananchi wa Kiburuki na Hifadhi ya Taifa ya Arusha ili tuweze kurudisha mahusiano?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo amesema ni kweli kwamba masuala yanayohusiana na migogoro ya mipaka baina ya maeneo yaliyohifadhiwa na maeneo wanayoishi wananchi yapo maeneo mengi katika nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa ya Arusha (Arusha National Park) ni mojawapo tu ya maeneo hayo, lakini nilikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba hivi tunavyozungumza ile Kamati ambayo tayari ilikwishaundwa inayoshirikishwa Wizara zaidi ya nne bado inaendelea na zoezi lake, watakapokuwa wamekamilisha kazi yao watakuwa wametoa ushauri Serikalini kuhusu namna bora zaidi ya kushughulikia migogoro hii ambayo tumekuwa tukiishughulikia kwa miaka mingi, lakini pengine tulikuwa hatujapata dawa ambayo ni sahihi. Sasa wakati tunasubiri kamati hii ikamilishe kazi yake pengine itakuwa si jambo
muhimu sana kwenda mahali ambapo pengine Kamati hii itakuwa imekwenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nafikiri itakuwa ni bora zaidi mimi na Mheshimiwa Nassari baada ya kuwa nimewauliza Kamati wamefikia wapi kama ni suala la kwenda kuona mimi na yeye tunaweza kwenda kama itasema kwamba bado haijakamilisha zoezi hili kwenye eneo analolizungumzia.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii, pia nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Lakini pamoja na majibu hayo mazuri nina maswali madogo tu ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ya Maliasili kupitia TFS imekuwa ikitoa vibali vya kuvuna mazao ya misitu. Mvunaji anaanzia vijijini, Wilayani kwenye kanda na hadi Wizara, lakini kabla ya kuruhusiwa kuvuna mazao ya misitu, Serikali imekuwa ikiwasajili wadau hawa na kuwatoza pesa kila mwaka. Vilevile kumekuwepo na tatizo kubwa la Wizara hii kuwa ikishatoa vibali hivi inachukua muda mfupi tu kuvifuta kama ilivyokuwa mwaka huu ambapo vilitolewa vibali zikiwemo approval za…
… kutoka nchi za nje na baadae vilifutwa na Mheshimiwa Waziri, sasa swali.
(a) Je, ni lini Serikali itaacha utaratibu huu mbaya na ambao unawatia hasara wadau wao?
(b) Serikali haioni sasa ni vyema isitoe approval hizi hadi ijiridhishe kwamba wananchi na wadau hawa wakipewa vibali hivyo watafanya kazi kwa mwaka mzima kuliko kama hivi wanatoa na kufanya kazi kwa miezi miwili tu na kuwasimamisha?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi suala la uvunaji wa maliasili linatokana na ukweli kwamba nia na dhamira ya Serikali ni kuliwezesha Taifa hili kuweza kutekeleza mipango yake yote ya maendeleo kwa kutumia rasilimali za Taifa hili ikiwemo maliasili. Jambo la msingi ni kwamba tunatakiwa kutumia maliasili hizo kwa namna ambayo ni endelevu. Kwa hiyo, udhibiti haumaanishi kwamba rasilimali hizi au maliasili hizo zisitumike kabisa, hapana, nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba tunafanya matumizi endelevu ili tuweze kuendana hata na malengo ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kuhusu swali lake moja kwa moja la utaratibu wa utoaji wa vibali, huo ni utaratibu ambao utatuwezesha kutoa fursa kwa kila mwananchi ya kuweza kushiriki katika uvunaji wa raslimali hizo. Lakini ikiwa kwamba, utaratibu huo unaonekana pengine una kasoro basi kwa kuwa ulikuwepo kwa mujibu wa sheria basi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anayo fursa ya kufuata utaratibu wa kawaida wa kuleta maoni ili tuweze kupitia upya sheria hiyo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kunipa nafasi. Niseme wazi kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza kwamba wananchi wa Sikonge wemesikitishwa sana na majibu ya Serikali. Ninayo maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kutumia takwimu za Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) za mwaka 2012 kama zilivyo ni sahihi, lakini je, Serikali haioni kuwa kutumia takwimu hizo bila kufanya projections kwa kutumia formular rasmi iliyo kwenye taarifa ya uchambuzi ya NBS inaweza kusababisha takwimu zisizo sahihi kwa mwaka 2017 na hivyo kusababisha Bunge hili pamoja na wananchi kuamini kuwa Serikali imelidanganya Bunge pamoja na wananchi? Hilo la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa kuwa takwimu rasmi zilizoko kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya ya Sikonge pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, ambazo pia ndizo alizonazo Mkuu wa Idara ya Maliasili wa Halmashauri inaonyesha kwamba kati ya kilometa za mraba 27,873 za Wilaya ya Sikonge, kilometa za mraba 26,834 ambayo ni sawa sawa na asilimia 96.3 ni hifadhi za misitu, wanyamapori, mapori ya akiba na maeneo mengine ya hifadhi ambayo yote hayo yako chini ya udhibiti na dhamana ya Kisheria ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Je, wananchi tumebaki na kilometa za mraba elfu moja na thelathini na...
…hili la pili, Serikali itateua lini timu yake ije kufanya kazi na timu yetu Sikonge, ili kusudi tupate suluhisho la kudumu kuhusu takwimu hizo?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, takwimu huwa zina chanzo, na mara nyingi unapokuwa unataka kunukuu takwimu ni lazima useme chanzo cha takwimu hizo yaani hizo takwimu ni kwa mujibu wa nani aliyezifanya. Takwimu zina mwenyewe na mwenye takwimu ni lazima awe ni mtu mwenye mamlaka na kwa Taifa hili takwimu ni mali ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, takwimu nilizozitumia kwa kuwa ni za Mtakwimu Mkuu wa Serikali sina shaka kwamba takwimu hizi ni sahihi na hizi ndizo takwimu zinazotakiwa kutumika
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kufanya projections kwamba ilitakiwa kuzitoa kutoka mwaka 2012 kuzileta leo, hiyo inaweza kuwa ni hoja, lakini ingekuwa ni hoja tu kama kweli hoja ya takwimu ingekuwa ni ya msingi kutokana na swali la msingi lililoulizwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ifahamike kabisa kwamba nchi yetu ndio nchi inayoongoza duniani kwa kuwa na eneo kubwa lililotengwa kwa ajili ya uhifadhi kwa ajili ya wanyamapori, misitu na hifadhi nyingine. Sisi tumetenga asilimia 25 ya eneo zima la nchi yetu, hiyo inatosha kutuma ujumbe kwamba ni kweli tumehifadhi maeneo makubwa. Lakini hatukufanya hivyo kwa makosa, tulifanya hivyo kwa sababu za msingi ambazo ndio zimekuwa zikitupa faida nyingi sana zinazotokana na uhifadhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tunapozungumzia uhifadhi kwenye eneo la Sikonge ifahamike kabisa kwamba uhifadhi huo sio kwa ajili ya Sikonge. Kila eneo lililohifadhiwa hapa nchini limehifadhiwa kwa maslahi ya Taifa. Eneo hilo litaweza kupitiwa pale ambapo kama Taifa tutaona kwamba kweli kuna haja ya kufanya mapitio.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimuombe Mheshimiwa Mbunge, pamoja na kumpongeza kwamba yuko hodari wa kufuatilia masuala yanayohusu wananchi wake, na yeye atakumbuka vizuri kabisa kwamba mwanzoni mwa mwaka huu tulikuwa wote Sikonge, tumepita kwenye maeneo yake, nami napenda wananchi wa Sikonge wajue kabisa kwamba wanao jembe, Mbunge wao ni mfuatiliaji sana wa masuala yanayohusu wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati huo huo nataka nimuombe kwamba atumie fursa hiyo ya kuwakilisha wananchi kwa kuwaambia ukweli kwamba akiba ni akiba na tunatakiwa kuyahifadhi maeneo yale kama akiba. Tutaweza kuyatumia pale tu itakapotokea kwamba kuna ulazima wa kuweza kufanya vinginevyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Serikali kuteua timu, nirudie tu kwamba tayari timu ipo na iko kazini na inaendelea na kazi hiyo, kinachosubiriwa sasa hivi ni wao na ile kazi yao kukamilika na kuweza kuleta mrejesho Serikalini kwa ajili ya kuweza kupiga hatua kutekeleza masuala haya yanayohusiana na upitiaji upya wa kile ambacho tunacho hivi sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho kabisa niseme kwamba kamwe Serikali haitaweza kufikia mahali ikaamua tu haraka haraka kuweza kuyaondoa maeneo yaliyohifadhiwa kwa matumizi mengine bila kufanya tathmini ya kuangalia kwamba maeneo yasiyohifadhiwa yametumika kwa tija. Kwa hiyo, jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba maeneo ambayo hatujahifadhi yanatumika kwa tija kwanza ndipo tuanze kugusa maeneo ambayo yamehifadhiwa kwa ajili ya akiba ya Taifa hili kwa ajili ya kizazi kijacho.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu marefu ya Mheshimiwa Waziri, lakini naomba nimuulize maswali mawili ya nyongeza. Nchi yetu imejaliwa kuwa na vivutio vingi vya utalii na ni dhahiri majibu ya Mheshimiwa Waziri inaonesha nchi yetu inaona utalii ni mbuga na wanyama tu; na ni dhahiri kwamba ukanda wa bahari unawekwa katika majibu kuonekana tu kama nao upo. Ni dhahiri pia kwamba nchi yetu sasa hivi ina eneo kubwa la bahari kuanzia Tanga mpaka Mtwara lakini utalii wa baharini kama diving, fishing na snorkeling unakua kwa kasi na una fedha nyingi sana. Je, Serikali ina mpango gani madhubuti sasa wa kukuza utalii wa baharini katika nyanja hizo za fishing, diving na snorkeling? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kuna matatizo makubwa ya upatikanaji wa umeme na maji katika maeneo ya uwekezaji na hili wawekezaji wanalalamika sana hata huko ambako unasema kwamba TANAPA wanafanya kazi pamoja na Ngorongoro. Wawekezaji wanalalamika kwamba kuna urasimu mkubwa wa kupata vibali vya uchimbaji wa visima au kupeleka umeme kwa ajili ya kutumia katika hoteli zao. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kweli kabisa wa kuondoa urasimu na gharama kubwa kwa wawekezaji katika kupata huduma hizi muhimu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kama amesikia vizuri kwenye jibu langu la msingi nilipokuwa nazungumzia diversification of tourism products (utanuaji wa wigo wa vivutio vya utalii), kwa bahati mbaya kwenye swali la msingi alisikia Ngorongoro na Hifadhi za Taifa za TANAPA akasema ni wanyamapori tu peke yake, lakini ukweli ni kwamba pale Ngorongoro tuna kivutio kikubwa sana ambacho kina sifa kubwa duniani na sasa hivi ni mwelekeo wa watalii wengi sana kuja kuona chimbuko la binadamu duniani ambayo si wanyamapori, hilo ni suala tu la kihistoria.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu suala lake la kukuza utalii katika maeneo mengine, ametaja mfano mmoja tu wa eneo la fukwe za bahari. Huo ni mpango wa Serikali na tayari tumekwishafanya kazi ya awali ya kufanya tathmini ukanda mzima wa bahari kutoka Tanga mpaka Mtwara jumla ya kilometa 1,000 na tumebaini maeneo kadhaa ambayo yana umiliki wa aina mbalimbali, maeneo mengine yanamilikiwa na watu binafsi na watu kama hao. Kwa hiyo Serikali iko kwenye mpango wa kuweza kuangalia namna bora zaidi ya kuweza kuelekeza uwekezaji kwenye maeneo hayo ili tuweze kuweka vivutio hivyo vya diving, fishing, snorkeling na aina nyingine ya utalii wa bahari na utalii wa fukwe.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la upatikanaji wa umeme na maji. Kwa ufupi kabisa, Serikali inayo taarifa juu ya changamoto hizo kwenye eneo hilo na tunachokifanya sasa hivi ni kushirikisha Serikali kwa ujumla wake; Wizara inayohusika na mambo ya umeme na ile inayohusika na maji, lakini pia kushirikisha wadau wa sekta binafsi wanaokwenda kuwekeza kwenye maeneo haya ya hifadhi ili tuweze kuona namna bora zaidi ya kurahisisha kuondoa urasimu, lakini pia kuwapunguzia walaji bei ya huduma hizi.
MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi ya upendeleo. Napenda kuuliza swali la nyongeza kwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Mkoa wa Mara ni kati ya mikoa iliyobarikiwa kuwa na vivutio vya utalii vikubwa ikiwemo Mbuga ya Serengeti kwa upande wa mashariki (Easten Corridor) lakini pia upande wa magharibi (Western Corridor). Je, ni nini mkakati wa Serikali kwa upande wa Western Corridor ambao imeonekana umesahaulika lakini una vivutio vingi vya utalii especially kwenye Ziwa Victoria lakini pia kuna visiwa? (Makofi)
Ina mpango gani wa kuendeleza utalii katika corridor ya Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, historia huwa inaandikwa namna hii na mimi nakuwa ni Naibu Waziri wa kwanza kujibu swali la kwanza kutoka kwa Mbunge, Mheshimiwa Catherine Ruge. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nampongeza kwanza Mheshimiwa Mbunge na napenda kumkaribisha katika jitihada hizi za kuweza kuwahudumia wananchi. Kuhusu swali lake la nyongeza kwa ufupi kabisa. Western Corridor anayoizungumzia ikiwemo eneo linalopakana na Serengeti upande ule wa magharibi, lakini pia Ziwa Victoria pamoja na visiwa vingine vyote ambavyo Mkoa wa Mara ni sehemu yake. Haya ni maeneo ambayo tayari Serikali imeshaweka mipango thabiti kabisa ya kuyaboresha.
Mheshimiwa Spika, hasa kuhusiana na Serengeti yako malango ya kuingia Serengeti yaliyozoeleka, mengi yanatokea upande wa Mkoa wa Arusha, lakini tumekwishaangalia hili na sasa kutokea Mkoa wa Mara, lakini pia kutokea Mkoa wa Shinyanga, tunakwenda kuboresha mageti ili tuweze kuwaruhusu watalii waingie kutoka kwenye kona zote zilizopakana na Serengeti ili kuweza kuruhusu idadi kubwa zaidi ya watalii kuingia katika maeneo haya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi, tuko mbioni kuboresha maeneo hayo na wakati wowote ule tunamkaribisha Wizarani kuja kuleta maoni kwa ajili ya kuboresha utalii. (Makofi)
MHE. LUCY F. OWENYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Katika Jimbo la Hai kuna kivutio cha Bwawa moja ambalo lina maji ya moto linaitwa Chemka. Wageni wamekuwa wakienda kule, lakini wanafika kwa kutumia kama vile njia za panya, lakini Serikali kama Wizara bado hawajakitambua kivutio kile na barabara ya kwenda kule ni mbaya sana. Swali langu, je, Serikali mpo tayari kwenda kukitembelea kituo kile cha maji ya moto na kukifanya official ili Serikali nayo iweze kupata mapato? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tu anazungumzia juu ya kivutio ambacho kiko kwenye Wilaya ya Hai...
Tuko tayari kwenda kukagua lakini nilitaka kuweka nyongeza...
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kilometa 180 tu kutoka hapa kuelekea Kondoa – Irangi kuna malikale nzuri, kuna michoro ya mapangoni na miundombinu ya barabara imeimarika. Sasa nataka kujua Wizara hii husika itatengeneza vipi yale mazingira ya kule ili kuimarisha utalii pamoja na mafunzo katika mapango ya michoro ya kale Kondoa – Irangi? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi vivutio vyote vya utalii ambavyo vinaangukia kwenye eneo la heritage tourism vyote tumefanya utaratibu wa kuviorodhesha halafu baadaye tunavisajili. Kuvisajili maana yake ni pamoja na kuangalia viwango vyake vya ubora na kuona kama kweli vinakidhi haja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa tumepokea taarifa hizo kutoka kwenye Wilaya mbalimbali, baadaye hatua inayofuata ni kuvitembelea na kuvihakiki.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Hata Wilaya ya Karagwe tuna vivutio vingi vya malikale likiwemo eneo ambalo Chief Rumanyika alikaa. Je, Wizara imeweka vivutio vya malikale hizi kwenye orodha ambayo Mheshimiwa Waziri ameitaja?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kivutio kinachohusu makazi ya Chifu Rumanyika ni moja tu kati ya vivutio vinavyohusu Machifu wetu wote nchi nzima kila eneo na kila Wilaya. Kwa hiyo, mpango wa Serikali ni kama nilivyoeleza hapo awali kwamba ni kuviorodhesha, kuvisajili, kuvikagua na kuona ubora wake na hatimae kuviuza kwa kuangalia sifa zake.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la moja. Kwa sababu Mheshimiwa Waziri ameonesha utayari wa kutembelea vivutio mbalimbali na kimsingi hajakuwa na ziara hivi karibuni ya kutembelea Nyanda za Juu Kusini ili akajionee maporomoko ya pili Afrika ya Kalambo pamoja na Ngome ya Bismark iliyoko Kasanga. Je, katika mwezi huo Agosti aliojipanga atatembelea na Nyanda za Juu Kusini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ukanda wa Kusini ni eneo ambalo sasa hivi kama Taifa tunaliangalia kuwa ni eneo la kupanua shughuli za utalii nchini kwa maana ya kufanya kwamba utalii sasa unakwenda kila eneo nchi nzima na si upande wa Kaskazini peke yake. Kwa hiyo, kwa ufupi jibu ni kwamba; kipindi hicho kitakapofika tutatembelea pia Ukanda wa Kusini ikiwa ni pamoja na maporomoko ya Kalambo.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niulize maswali mawwili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wangu wa Kata za Kisiwani, Vumari na Mji Mdogo wa Same wamebanwa sana na Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi; na kwa kuwa Mwenyezi Mungu wakati anaumba dunia alimuumba binadamu akamwambia atawale viumbe vyote viishivyo kwenye maji na kwenye nchi kavu; na kwa kuwa wakati wa uhuru tulikuwa na idadi ya watu milioni 10.3 na sasa hivi tuko takribani milioni 50, tulikuwa na ng’ombe milioni nane sasa hivi milioni 28; tulikuwa na mbuzi milioni 4.4 sasa hivi ni milioni 16.6; tulikuwa na kondoo milioni tatu na sasa hivi ni milioni tano, tulikuwa na nguruwe 22,000 sasa hivi ni milioni mbili, astaghfilillah nimetaja nguruwe wakati ni mwezi wa Ramadhani, mnisamehe sana. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza je, Wizara ya Maliasili na Utalii iko tayari kushirikiana na Wizara ya Kilimo, TAMISEMI pamoja Ardhi ili waweze kutathmini eneo na idadi ya watu pamoja na mifugo wanayofuga ili kusudi kama kuna uwezekano maeneo ya hifadhi za misitu pamoja na Hifadhi za Wanyamapori zipunguzwe ili binadamu waweze kupata maeneo ya makazi pamoja na mifugo na kilimo?
Swali la pili, kwa kuwa Botswana, Afrika ya Kusini na Namibia wameweza kuzuia wanyamapori kutoka kwenye mapori kwenda kwa binadamu ama kwenye wanyama wanaofugwa, je, Serikali iko tayari sasa kuandaa mpango rasmi wa kuweka fence ili wanyamapori wasiweze kwenda kwenye makazi ya watu kuwasumbua na kuwaletea madhara ikiwa ni pamoja na vifo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza Mheshimiwa Mbunge anazungumzia upungufu wa ardhi kwa ajili ya matumizi ya kibinadamu hasa kwa ajili ya faida ya kiuchumi na kijamii, akihusisha na uhaba au upungufu wa rasilimali ardhi kwa ajili ya shughuli hizo zinazotokana na ongezeko la binadamu na wanyama kama ambavyo amewataja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi Serikali inatambua na kwa kweli ni dhamira ya Serikali kuwafanya wananchi waweze kufanya kazi za kuzalisha mali kwa sababu ni kwa kufanya hivyo tu peke yake ndiyo hata madhumuni makubwa kabisa ya Serikali ya kuiondoa nchi kutoka katika uchumi wa chini kwenda uchumi wa kati yatafanikiwa, ni kwa kufanya kazi tu peke yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili wananchi waweze kufanya kazi lazima waweze kuwa na ardhi au wawe na maeneo ya kufanyia kazi. Kabla hatujaanza kusema kwamba maeneo tunayoyatumia hayatoshi ni lazima kwanza tuone maeneo hayao yanatumikaje hivi sasa, kwa hiyo, hapa ndipo ambapo tunazungumzia juu ya suala la mpango wa matumizi bora ya ardhi.
Kuhusu swali lake tutashirikiana vipi na Wizara nne zile alizozitaja ukweli ni kwamba Mheshimiwa Mbunge anafahamu kwamba tayari tunayo Kamati ya Kitaifa ya Wizara alizozitaja ambayo iko kazini inashughulikia suala hilo na baada ya utafiti wa kitaalam, baada ya kujiridhisha kitaalam tutapitia upya sheria na kuona katika kila eneo kama kweli suluhisho pekee la kuweza kuwafanya wananchi kupata eneo la kufanya shughuli za kibinadamu kama suluhisho pekee ni kugawa maeneo ambayo yamehifadhiwa kwa faida ambazo tunazifahamu ziko lukuki, basi Serikali itazingatia mwelekeo huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kutajitokeza ukweli kwamba bado maeneo tuliyonayo tunaweza kuyatumia vizuri zaidi bila kuathiri maeneo yaliyohifadhiwa basi hatutakuwa na haja ya kupunguza maeneo ya hifadhi isipokuwa tutajiimarisha zaidi katika kutumia vizuri zaidi maeneo ambayo hayajahifadhiwa kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili juu ya kuweka fence, kuweka uzio kwa ajili ya kuzuia wanyamapori kwenda kwenye maeneo ambayo ni ya binadamu, kwa ajili ya maeneo ya makazi ya binadamu na maeneo ambayo binadamu wanafanya shughuli za kibinadamu za kiuchumi na kijamii; napenda tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba huko ambako anazungumzia kwamba udhibiti umefanikiwa njia iliyotumika siyo hii tu peke yake ya kuweka fence, njia ya kuweka fence ni njia mojawapo na inatumika tu pale ambapo ni lazima kuweka fence kwa sababu njia hii ni ya gharama kubwa na si rafiki pia kwa mazingira hata kwa wanyama wenyewe na hata kwa binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kwa sasa hivi ni kwamba Serikali inalichukua suala hili na kwa kweli tumekuwa tukilifanyia kazi muda mrefu kuweza kuona ni namna gani tunaweza kudhibiti kiwango na kasi ya Wanyamapori kutoka kwenye maeneo yao na kwenda kwenye maeneo ambayo ni ya binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la msingi hapa vilevile na binadamu na wenyewe tusiendelee na utaratibu ule wa kwenda kukaa kwenye maeneo ambayo aidha ni njia za wanyapori au ni maeneo ya mtawanyiko ya wanyamapori.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la hifadhi ya Mlima Kilimanjaro una eneo la Half Mile au 0.8 ya kilometa, huduma za jamii kwa mfano uvunaji wa majani, uvunaji wa kuni kusafisha vyanzo vya asili vya maji, kwa mfano mifereji, inahusu vijiji 42 vya Halmashauri ya Wilaya ya Moshi. Wakati huu hakuna mahusiano mazuri kati ya wananchi wa vijiji hivi 42 pamoja na Hifadhi chini ya KINAPA hasa wale askari. Serikali haioni ni vema pande zote zinazohusika yaani wawakilishi wa vijiji pamoja na KINAPA ikisimamiwa na Serikali kuweka taratibu na kanuni endelevu zinazoaminika za mazingira ya kisasa ili mahusiano mema kati vijiji 42 na Hifadhi ya Mlima Kilimajora viweze vikawa vya mazingira ya kisasa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi kabisa Serikali inazingatia ukweli kwamba ili uhifadhi uwe endelevu ni sharti wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi husika, wanaopakana nazo waweze kuona kwamba wao ni sehemu ya huo uhifadhi kwenye hayo maeneo yanayohusika.
Kwa hiyo, njia zote zinazotumika katika kukamilisha malengo ya uhifadhi ni lazima ziwe rafiki kwa wananchi ambao wanazunguka kwenye maeneo hayo. Kwa sasa Serikali inachokifanya ni kuanzisha taratibu za kuwasogelea wananchi kwa ukaribu kabisa na kuwashirikisha, kuwapa elimu kwanza ya manufaa ya uhifadhi wenyewe, pia kuona namna gani wanaweza kushiriki kwenye jitihada za Serikali za kuhifadhi, muhimu zaidi mwishoni kabisa ni kuona namna ambavyo wananchi hawa wanaweza wakanufaika na uhifadhi moja kwa moja ukiacha ule utaratibu wa kunufaika na uhifadhi kwa njia na taratibu za kawaida za Kiserikali.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wakati anajibu suala la Mbuga ya Mkomazi na Mbuga ya Mkomazi kwa Mkoa wa Tanga kuna Wilaya ya Lushoto, Korogwe na Mkinga. Tatizo la mipaka hata kule linatuathiri na kuna timu sasa inapita kutathmini hilo tatizo, nataka nitambue, je, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili imeshirikiana na hawa watalaamu ambao wanapita kutathmini ile mipaka, hasa katika eneo la Mwakijembe Wilaya ya Mkinga?

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mbuga ya Mkomazi kwa Mkoa wa Tanga iko katika Wilaya za Lushoto, Korogwe na Mkinga na hili tatizo la mipaka sasa hivi kuna timu ya ambayo iko chini ya RAS kwa kule Tanga inafuatilia haya maeneo yenye migogoro ambayo wananchi na mbuga wanakinzana hasa eneo la Mwakijembe katika Halmashauri ya Mkinga, je, Wizara ya Maliasili na Utalii inatambua uwepo wa hii timu ambayo inakagua mipaka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa timu hiyo inayokagua mipaka.
Lakini Mheshimiwa Mbatia nafikiri wakati nikiwa namjibu swali alikuwa anasisitiza lini nilimuona wakati anataoka alikuwa anaendelea kuongea anauliza lini, sasa Mheshimiwa Mbatia tukimaliza kikao hiki cha Bunge (Kamati ya Fedha hivi) mimi na wewe tuambatane tukaangalie uhalisia ulivyo halafu tuweke ratiba ya kushughulikia suala hilo.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mheshimiwa Waziri anasema kwamba mpango mkakati mmojawapo ni kutangaza kuingiza hiyo tovuti na filamu. Hapa swali lilikuwa linataka kujua mkakati thabiti wenye dhamira ya kweli kwa sababu hapo wanaposema, hata barabara ya kufika kwenye hivyo vivutio hakuna. Sasa huu mkakati, hata hao watu unaoingiza kwenye filamu, watafikaje kule Kilwa ambapo kwenye hivi vivutio hamna barabara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba Pwani ya Afrika Mashariki ni mahali ambapo kwanza walikuwa na currency yao, yaani walikuwa na pesa yao; ni Kilwa, lakini haya yote watu hawayajui.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kwa mfano, ukiangalia Vita ya Majimaji; asili ya vita hii ni Kilwa, lakini makumbusho ya Vita ya Majimaji yako Songea. Sasa Wananchi wa Kilwa walitaka waone, Serikali inafanya taratibu gani kuirudisha Vita ya Majimaji Kilwa na kuitangaza Kilwa kama sehemu ya Utalii? Hilo ni swali la kwanza.(Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mheshimiwa Kuchauka nafikiri wewe na mimi kwa pamoja tunafahamu kwamba historia ya kwamba Kilwa haifikiki au haipitiki ilikuwa labda zamani; lakini kwa sasa hivi ninavyofahamu na nafikiri Wabunge wengi wanafahamu, kama unazungumzia barabara ya kufika mpaka Kilwa; ni ya lami, kwa maana vivutio vya Mjini Kilwa, yale magofu pamoja na maeneo mengine ya utalii wa kiutamaduni pamoja na utamaduni wa kihistoria.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama anazungumzia Mbuga ya Selous, kufika ndani ya Hifadhi ya Selous, ni kweli kuna namna na haja ya kuboresha miundombinu ya kufika ndani ya Selous na kuzunguka ndani ya Selous yenyewe kwa maana ya barabara; lakini iko miundombinu ambayo ni maeneo ya malazi au facilities za malazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, upande mmoja ni jukumu la Serikali, kwa mfano kama barabara, lakini upande mwingine ni jukumu la taasisi binafsi ambazo sasa Mheshimiwa Mbunge usaidie Serikali mnapokaa kwenye Mabaraza kule ya Halmashauri kuweza kuona namna ambavyo mnaweza mkashirikiana na Serikali kuweza kuhamisha wawekezaji wakaweza kuweka vivutio ndani ya Selous.
Mheshimiwa Naibu Spika, pengine nimtaarifu tu Mheshimiwa Kuchauka kwamba mkakati anaoutaka mahususi sasa kwa ajili ya Kilwa yenyewe; sasa hivi tunakamilisha hadidu za rejea kwa ajili ya mkakati mahususi kabisa kwa ajili ya Kilwa. Siyo Kilwa peke yake, kwa ajili ya southern circuit. Huu ni utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Miaka Mitano ambao tunaposema kutekeleza Mpango wa Miaka Mitano, maana yake tunazungumzia diversification kwamba kutanua wigo wa vivutio vya utalii nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kupitia mkakati huo, tuna uhakika kwamba tunakwenda kuboresha mazingira ambayo yataboresha utalii ndani ya Selous lakini pia vivutio ambavyo viko Kilwa Mjini hasa vya utamaduni na kihistoria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Vita ya Majimaji, hilo suala bado linajadiliwa. Wako upande mmoja katika Kambi nyingine wanasema ni muhimu zaidi kuzingatia kwamba historia ya Majimaji ina mizizi zaidi Kilwa, wengine wanasema ina mizizi zaidi Songea. Sasa nafikiri unatingisha kichwa kwa sababu hayo ni maoni yako, lakini nafikiri suala hili linajadilika, lakini hali ilivyo kwa sasa hivi, mazingira yaliyoko sasa hivi yanazingatiwa kwa mujibu wa historia hiyo hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri utakumbuka siku za nyuma tulikaa hapa tukawa tunazungumzia kuhusu suala la historia kwamba wengine wanasema historia inabidi ziandikwe upya, lakini hatuna sababu ya kuandika upya, lakini tutaweza kuweka utaratibu ulio makini kuweza kuweka suala hilo likakaa sawa.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Spika, kwa fursa. Wilaya ya Kondoa hususan pale Kata ya Kolo na nyinginezo, ipo michoro ya mapangoni ambayo ni vivutio vikubwa sana vya kihistoria kwa ajili ya utalii, lakini vimekuwa havitangazwi sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuvitangaza ili kizazi cha sasa na cha baadaye kitambue hii fursa na kuweza kuitumia ili hatimaye pia kipato kiongezeke?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, michoro ya kwenye mapango ya Kondoa ni mojawapo kati ya maeneo ya utalii wa kiutamaduni na utalii wa kihistoria ambao tayari unafahamika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ambayo imebaki sasa hivi ni ya kuweza kuboresha matangazo kwa maana ya utangazaji wa utalii; na nimesema katika majibu yangu ya maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Kuchauka, kwamba tunachokifanya sasa hivi ni utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao unasisitiza juu ya diversification of tourist attractions, kwamba tunataka kuendelea kuboresha na kutanua wigo wa vivutio vya utalii ili tuondokane na vivutio vya utalii vinavyohusiana na wanyamapori peke yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, chini ya mpango huu, chini ya utekelezaji wa Mpango wa Miaka Mitano, tunakwenda kutangaza zaidi vivutio ambavyo ni vipya; vimekuwepo lakini vimekuwa havitiliwi mkazo, lakini sasa tunakwenda kuvitilia mkazo kwa maana ya kwamba tutaboresha zaidi matangazo kwa ajili ya vivutio vya aina hiyo.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kule Moshi Vijijini kuna vyanzo vingi vya kitalii ambazo havijatangazwa vizuri. Kwa mfano, kule Kata ya Uru Mashariki kuna maanguko ya maji ya ajabu sana yanaitwa Mnambeni na hivi karibuni katika Kata ya Mbokomu, kumevumbuliwa mti ambao unasemekana ni mrefu kuliko miti yote katika Bara la Afrika. Sasa nataka kufahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itachukua hatua za makusudi kuweza kuvitambua hivi vyanzo na kuvitangaza inavyostahili ili tuweze kuvitumia kikamilifu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu hii ni tajiri sana ya vivutio vya utalii. Kama nafasi ingekuwepo, karibu kila Mbunge hapa angeweza kusimama na kueleza kwamba katika Halmashauri yake kuna kivutio hiki na kile; sasa suala la kuboresha utangazaji siyo suala la Serikali peke yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali inaendelea na utaratibu wa kuweza kuboresha matangaza ambayo sasa hivi tunafanya, nitoe wito sasa kwa Mbunge moja moja lakini kupitia Halmashauri zinazohusika kuanza kuvibainisha vivutio vilivyopo kwenye maeneo yao ili viweze kwenda mbele ya wataalam wa Idara ya Utalii katika Wizara ya Maliasili na Utalii tuweze kuviorodhesha kwa pamoja, halafu tukubaliane kama vinakidhi viwango vya Kimataifa kama vivutio, tuweze kuvifanyia grading, halafu baada ya pale tuendelee na utaratibu wa kutangaza tukitambua kwamba ni jukumu letu sote.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 mwananchi mmoja wa Kenya alitamka maneno kwenye mkutano mmoja wa Kimataifa kwenye nchi mojawapo nje kule, kwa kurusha tu clip ndogo tu lakini ikatingisha dunia, lakini pia na sisi Watanzania tukaanza kusema kwa nini wanataka kuteka vivutio vyetu? Ule haukuwa mpango wa Serikali, ni mtu mmoja tu alifanya vile.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wananchi wa Tanzania nasi kwanza tushiriki katika utalii wa ndani ili tuvifahamu vivutio vyetu na sifa zake halafu baada ya pale nasi tuweze kushiriki kama Watanzania kutangaza vivutio vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza kushirikiana na wenzetu walioko nchi za nje kwa utaratibu wa diaspora ili tuweze kufanya nchi yetu ikapata kutangazwa sawa sawa kwa maana ya vivutio vya utalii. (Makofi)
MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kule Wilayani Mbinga yako mawe mawili makubwa ya ajabu ambayo yanafahamika kwa jina la Mawe ya Mbuji; mawe haya yanasadikika kuwa ni jiwe la kike na la kiume; lakini pia katika mawe hayo viko viumbe hai vyenye kimo kifupi sana vinavyofanana na binadamu, viumbe hivi huwa vinajitokeza hasa msimu wa michezo ya utamaduni. Je, ni lini Serikali itafanya utafiti ili kubaini ni viumbe vya aina gani hivyo ambavyo vinaishi katika mawe hayo na hatimaye kutangaza eneo hilo kama eneo la utalii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye maswali ya nyongeza yaliyotangulia, nimesema nchi hii ni tajiri sana ya vivutio vya utalii, jambo ambalo hatujalikamilisha bado na tunaendelea kulifanya ni kuwa na orodha ya vivutio hivyo vilivyohakikiwa kwa sababu siyo kila kitu ambacho mtu mmoja anaweza kukiona kwamba kinatosheleza kuwa kivutio cha utalii, kinakuwa hivyo; ni mpaka wataalam wanaohusika waseme kwamba sasa hiki kinakidhi viwango vya Kimataifa vya kuwa kivutio cha utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii, tayari imeshawasiliana na Halmashari zote nchini ili kuweza kuviorodhesha vivutio hivyo, vifike Wizarani, tuvifanyie uchambuzi halafu tuweze kuviweka katika makundi (grading) halafu tuweze kuweka mkakati wa pamoja wa namna gani ya kutangaza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema jukumu la kutangaza lisiwe jukumu la Serikali peke yake; kama mnavyofahamu na mnavyoona, dunia ya sasa ni kama kijiji; na kila mmoja akitumia wajibu wake wa kutumia mifumo ya mawasiliano ya kisasa, tunaweza kutangaza nchi yetu kwa namna ambayo ni ya mafanikio zaidi.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa nchi yetu ina maeneo mengi ya masalia ya Wafalme pamoja na majengo; kwa mfano, Mtemi Shomali Mwanansali wa Igurubi, kuna majengo ya Mtemi Humbi Ziyota Mwanantinginya pale Ziba. Kwa nini Serikali sasa isiyatambue maeneo haya yote yenye majengo na masalia ya Watemi nchini kote na kuyatangaza? Najua wenzetu kutoka Ulaya watakuja kuyaangalia. Ahsante sana.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo yalikuwa makazi au hata ni makazi hata sasa ya viongozi wetu wa kimila; Watemi, Mamwinyi na wengineo, kweli ni maeneo ambayo licha ya kwamba ni ya kihistoria, yana vivutio kwa sababu kimsingi yana record ambayo inaweza kutupa hata mafundisho kwa ajili ya siku za usoni. Kama ambavyo tunajua historia na faida zake, kwamba unaangalia tulikotoka, hapa tuliko na huko mbele tuendako, inaweza kuwa ni mchango mkubwa sana kwa upande wa maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza tukajiuliza, hivi ni kwa kiasi gani sisi wenyewe kwanza tunatembelea maeneo hayo? Ni kwa kiasi gani sisi wenyewe tunayapenda maeneo hayo na tunayatunza kabla hatujafikiria hata kuyatangaza kwa ajili ya watalii kutoka nje? Sasa wito nilioutoa kabla na napenda kuurudia tena hapa, tuanze sisi wenyewe kwanza kwenye Halmashauri zetu kuanza kuthamini maeneo hayo, kuyaweka vizuri katika ubora wake, halafu baada ya pale, kuwasiliana na Wizara ya Maliasili na Utalii na kuweza kuona namna gani tunaweza kuviboresha na kuvitangaza vivutio hivyo ndani na nje.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana nami kupata fursa hii ya mwisho ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa mazingira ya kusini katika maana ya Ruaha, Rufiji mpaka Kilwa yanafanana kabisa na Hifadhi ya Msitu wa Liparamba unaounganisha upande wa Nyasa, Mbinga Mjini na upande wa Msumbiji. Ni lini Hifadhi ya Liparamba itapata hadhi inayostahili ili iwe kivutio cha utalii kwa center ya Kusini, hususan tunaunganisha nchi mbili za Msumbiji na nchi ya Malawi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kwamba Hifadhi ya Liparamba iliyopo mkoani Ruvuma ni mojawapo kati ya maeneo ya hifadhi ya wanyamapori machache sana kwa Mkoa wa Ruvuma, lakini tajiri kwa wanyamapori na ambayo inastahili kabisa kuwa kwenye viwango vya Kimataifa vya kuwa mojawapo ya maeneo yenye vivutio vya utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli pia kwamba katika siku za nyuma, mkazo wa kuweka mipango na mikakati ya kuweza kuboresha utalii katika hifadhi hiyo, hapo nyuma hakukuwa na mipango madhubuti kwa sababu hatukuwa na utaratibu wa kuweza kuboresha utalii upande wa kusini mwa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hapo awali kwamba katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, tumezungumzia juu ya ku-diversify au kuweka utaratibu wa kuwa na mtawanyiko wa vivutio kwa maana ya vivutio vyenyewe; aina za vivutio, pia mahali vivutio vilipo hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, chini ya mpango huo, tutakwenda kuboresha utalii kusini na Hifadhi ya Liparamba ni mojawapo kati ya hifadhi ambazo zinaenda kuwekwa katika kipaumbele ili kuhakikisha kwamba sasa watalii hawaendi tu Arusha, Moshi, Kilimanjaro na maeneo ya Kaskazini, pia waweze kwenda Mbeya, Songea, Mtwara na maeneo mengine ya Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge atupe nafasi tuweze kukamilisha mipango iliyopo kwa ajili ya kutekeleza sehemu ya mpango wa miaka mitano ili tuweze kuona sasa tunaboresha utalii upande wa kusini.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake. Pamoja na Serikali kukiri kuwa zao la mbao linachangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa nchini, lakini barabara zinazoingia katika maeneo ya misitu ni mbovu sana na hazipitiki hasa wakati wa mvua. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka lami katika maeneo hayo ambako mbao hizo zinavunwa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa serikali imekuwa ikimuuzia mwekezaji wa nje (MPM Mgololo) nusu bei ya magogo, je, iko tayari sasa kuwauzia wajasiliamali wetu bei sawa na hiyo ili kuitikia wito wa uchumi wa viwanda. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Ritta kwanza kwa kuonesha nia na dhamira ya kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuendeleza viwanda nchini na hasa viwanda vinavyopata malighafi yake kupitia misitu; lakini pia nijibu maswali yake ya nyongeza mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza la uboreshaji wa miundombinu ya barabara. Kwanza ni jambo ambalo hata upande wa Serikali ni la interest, kwamba maeneo ya mashamba yaweze kupitika kirahisi kwa ajili ya kuweza kuyahudumia mashamba yenyewe. Hata hivyo kuhusiana na suala la barabara zainazokwenda kwenye mashamba yenyewe ambazo zipo kimsingi chini ya Halmashauri ya Wilaya, barabara za makundi haya mawili zinashughulikiwa kwa namna tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi barabara ambazo zipo chini ya Halmashauri; katika Halmashauri ambazo zina mashamba Serikali inachokifanya ni kuweza kuchangia nguvu na uwezo wa kuweza kuhudumia barabara hizo kupitia uazimishaji wa mitambo mbalimbali ya ujenzi wa barabara. Mahali ambapo Serikali za Halmashauri zenyewe huweka mafuta kwenye mitambo hiyo na kuwezesha ujenzi wa barabara hizo. Serikali itaendelea kutumia njia hiyo ili kuweza kuhakikisha kwamba barabara hizo zinaendelea kuwa bora zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa barabara za ndani, tutaendelea kuziboresha kama ambavyo tunaendelea kufanya. Nimshauri tu Mheshimiwa Ritta kwamba haiwezekani kufanya barabara hizo zikafikia kiwango cha lami kwa sasa kwa sababu ya majukumu mengine ya Serikali ya uendelezaji wa miundombinu katika maeneo mengine, hizi za mashambani zitakuwa bora lakini katika kiwango hicho hicho cha barabara za udongo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la mwekezaji wa Kiwanda cha Karatasi pale Mgololo (MPM); suala hili ni pana, kubwa na la kina na Serikali mara kwa mara imekuwa ikitoa maelezo kuhusu suala hili la mwekezaji huyu ambaye historia yake ni ndefu inaanzia wakati wa Sera ya Ubinafsishaji ya Taifa huko miaka ya nyuma. Hata hivyo, kwa hali ilivyo sasa maelezo ninayoweza kuyatoa hapa kwa sasa hivi ni kwamba kwanza ieleweke kwamba miti ambayo ilikuwa inauzwa au ambayo inauzwa kwa mwekezaji ni magogo yanayotokana na miti ambayo ni ya umri mdogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, umri wa uvunaji wa miti
kwa ajili ya bidhaa ya mbao ni miaka 25 na zaidi, lakini magogo haya ambayo yanauzwa kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa ambayo inakwenda kuwa malighafi kwa ajili ya uzalishaji wa karatasi inayoitwa pulp ni miaka kuanzia 14.
Kwa hiyo, si magogo yale yale ambayo anauziwa mwekezaji huyu ambayo wanauziwa wazalishaji wa mbao katika maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa ninachoweza kusema ni kwamba, kwa sababu ya kina cha maelezo katika suala hili, Mheshimiwa Waziri ameandaa maelezo ya kutosha kwa kirefu kuhusiana na suala hili kwa sababu ya kupokea hoja mbalimbali kutoka kwa wananchi wa maeneo hayo hayo na Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kuwa ameungana na wananchi wa maeneo hayo kutaka kujua ni namna gani wananchi wananufaika zaidi na Taifa linanufaika zaidi basi muipe fursa Serikali tuweze kupata nafasi Mheshimiwa Waziri atakuja kutoa maelezo ya kina zaidi katika wakati ambao ataweza kutoa maelekezo.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ninayo maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ajili ya mahusiano ya ujirani mwema TANAPA Mkoani Katavi wamejitolea kuchimba visima kwenye vijiji vitatu ambavyo ni Kijiji cha Matandarani, Igongwe na Stalike lakini condition yao ni wanakijiji wachangie 30%. Gharama ya hivyo visima ni milioni 21, asilimia 30 itakuwa kama kwenye shilingi milioni saba, wanakijiji watatakiwa wachangie ili waweze kuchimbiwa hivyo visima vitatu. Je, TANAPA ili kudumisha mahusiano mema na Mkoa wa Katavi na ukizingatia kwamba kule mkoani kwetu vipato viko chini, wananchi hawana uwezo wa kuchangia hiyo shilingi milioni saba, inaonaje ikachukua hiyo gharama ikachimba bila kuwachangisha wananchi?Hilo swali la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, ni lini TANAPA itajenga hoteli ya nyota tatu katika Mkoa wangu wa Katavi ili tuweze kupata watalii kutoka nje na ndani ya nchi? Nauliza hivyo kwa sababu mkoa hauna hoteli ya nyota tatu ambayo inaweza kuwawezesha wageni kutoka nje kuja kutalii mkoa wetu na kuangalia huyo twiga mweupe ambaye hapatikani duniani kokote isipokuwa Mkoa wa Katavi?Ukizingatia kwamba sasa hivi uwanja wetu ni mzuri…
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza la uchangiaji kwenye utekelezaji wa miradi ya ujirani mwema na nafikiri niweke vizuri tu hapa kwamba, TANAPA hawajitolei bali wanatekeleza wajibu wao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu kwamba pale ambapo kuna wananchi wanaishi jirani na maeneo ya hifadhi, mahali ambako utalii unafanyika tunao wajibu wa kuweza kutekeleza miradi mbalimbali chini ya utaratibu wa ujirani mwema.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango tulioweka wa kuchangia unawafanya wananchi waweze kwanza kushiriki moja kwa moja kwenye shughuli za uhifadhi lakini pia kujisikia kwamba na wenyewe ni sehemu ya uhifadhi lakini sehemu pia ya kufanya shughuli za maendeleo. Kwa hiyo, kwa kuwa utaratibu huu uko kwa mujibu wa kanuni, ikiwa Mheshimiwa Mbunge ana maoni bora zaidi ya haya aliyotuambia au ana namna bora zaidi ya kueleza kwa kirefu maoni hayo, basi anaweza kuyaleta Wizarani tukapitia utaratibu mzima wa utekelezaji wa miradi ya ujirani mwema.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, je, ni lini TANAPA itajenga hoteli ya nyota tatu Mkoani Katavi na kwa kweli anauliza kwamba kwa nini TANAPA wasijenge hoteli ya nyota tatu ili kuweza kuboresha shughuli za utalii Mkoani Katavi. Kwa ufupi tu ni kwamba, Serikali haijengi hoteli kwa ajili ya matumizi ya watalii au kwa ajili ya matumizi mengine yoyote kwenye sekta ya utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu la Serikali ni kuweka mazingira mazuri ya kuwawezesha wawekezaji ambao wanatoka private sector kuweza kuwekeza kwenye eneo hilo. Kwa hiyo, nimshauri tu Mheshimiwa Mbunge aungane na Serikali kuwashawishi wadau kutoka mahali popote pale waweze kuja kwenye Mkoa wa Katavi kuwekeza na kujenga hoteli si ya nyota tatu tu, hata kama wanaweza ya nyota nne, nyota tano, ili mradi kuwe na mazingira ambayo yatawawezesha watalii kuvutiwa na kuja kutalii wakiwa katika hali ambayo ni bora zaidi.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Je, Serikali baada ya kupata repoti iliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha kuhusu Pori Tengefu la Loliondo inampango gani wa kutoa suluhu ya kudumu kwenye mgogoro huu uliodumu zaidi ya miaka 20?
Swali la pili, je, Serikali inaweza kuahidi nini juu ya mgogoro huu wananchi wa Loliondo ili waweze kuendelea na kazi zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Catherine Magige Mbunge wa viti maalum Mkoa wa Arusha ambaye kwa kweli licha ya swali hili amekuwa akifuatilia kwa karibu sana juu ya masuala yanayohusiana na changamoto za Pori la Loliondo moja kwa moja akija kuhoji ofisini, lakini kuhusu maswali yake mawili ya nyongeza yote yanafanana kwamba hatua ambayo Serikali inaenda kuchukua ili kuwawezesha wananchi wa maeneo haya waweze kuendelea na shughuli zao kama ambavyo ameuliza.
Mheshimiwa Spika, Kama ambavyo nimejibu katika swali langu la msingi kamati iliyoundwa imefanya kazi kubwa ya kina kazi ambayo imezingatia maslahi ya pande zote upande wa wananchi lakini pia upande wa maslahi ya Taifa, lakini kwa kuwa ile ni taarifa ambayo ni ya kitaalam lakini pia iliyozingatia kama nilivyosema maslahi ya pande zote na kwa kuwa nimesema tayali iko kwenye dawati la Mheshimiwa Waziri Mkuu basi nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute subira Waziri Mkuu bila shaka atakuwa anaipitia kwa kutumia wataalam chini ya ofisi yake baada ya pale taarifa itakayotolewa itakuwa na maelekezo ya namna gani tunaweza kusonga mbele katika kutatua mgogoro huu. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa kuna kampuni ya OBC ambayo inamirikiwa
na mwarabu na imekuwa ikiwepo Loliondo kwa muda mrefu na wamekuwa wakifanya uwindaji, wamekuwa wakiangalia maslahi yao zaidi bila kuangalia maslahi mapana ya uhifadhi wa Bonde Tengefu la Loliondo. Ni kwa nini Serikali inamshirikiali au inamaslahi gani na huyu mwarabu amekaa huko kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo ulipata mashaka, lakini na mimi nilikuwa na mwelekeo huo huo, lakini hata hivyo kwa ajili tu ya kuweza kuboresha, niseme tu kwa kifupi kwamba kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, kamati iliyoundwa ile ya kitaalam ilihusisha makundi yote, wataalam lakini pia wawekezaji na wananchi. Unapohusisha makundi yote, basi kila jambo ambalo ni changamoto linajadiliwa kwa mapana na marefu wakati kamati ikiwa inafanya kazi. Ninaamini ndani ya taarifa ambayo iko kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, mambo yote ambayo yanahusiana hasa na wawekezaji, na napenda hapa tutumie lugha sahihi ya kuwa-address wawekezaji, na nafikiri jambo la msingi ni kwamba hawa ni wawekezaji wana haki zao nchini wa mujibu wa sheria, lakini kama yapo yale ambayo ni changamoto na yanatakiwa kufanyiwa kazi, basi hiyo ndiyo kazi ambayo kamati imefanya. (Makofi)
MHE. MBARAKA K. DAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mafia ina vivutio vingi sana akiwemo huyu samaki wa ajabu anayeitwa Potwe au whale shark. Vile vile Mafia kuna maeneo mazuri sana ya scuba diving, sports fishing na kuna fukwe tulivu. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri Mafia kama Wilaya mpaka leo haina Afisa wa Utalii. Sasa swali la kwanza, ni lini Serikali itatupatia Afisa wa Utalii katika Wilaya ya Mafia?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini Serikali itaruhusu
au itaifungulia ile hoteli ambayo Mheshimiwa Simbachawene alikuja akaifunga ya Chole Mjini, ambapo wananchi wanapata pale ajira, Serikali inapata kodi na wale wawekezaji pale walikuwa wanasomesha vijana wengi katika kisiwa cha Chole, sasa ni nini tamko la Serikali juu ya kuondoa tofauti zilizokuwepo ili ile hoteli iendelee kufanya kazi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza nakubaliana na yeye na Serikali inatambua kwamba, Mafia ni Kisiwa tajiri cha vivutio vya utalii; na kwa kweli Mafia ni mojawapo ya maeneo nchini ambayo yataiwezesha Serikali kufikia malengo yake ya ku-diversify, kutanua wigo wa aina ya vivutio, lakini pia kutanua wigo wa kufanya utalii maeneo mengi zaidi nchini kuliko maeneo machache ambayo yanaendelea hivi sasa. Kwa hiyo, ule umuhimu wa Mafia tayari Serikali inaufahamu na inaufanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na hoja yake ambayo ni ya msingi kabisa ya kwamba ili tuweze kufikia malengo katika hayo ni vema tukawa na Afisa Utalii kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mafia, nakubaliana naye. Hata hivyo, nimshauri tu Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili ni vema akaenda kulipeleka kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mafia ili waweze kuangalia kwa namna gani wanaweza kuingiza kwenye ikama nafasi hiyo ya Afisa Utalii.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la hoteli aliyoitaja, hoteli ya Chole pale Mjini Mafia, licha ya faida zote alizozitaja ni kweli Serikali inafahamu kulikuwa na fursa za ajira za wananchi na faida nyingine kama ambavyo ameweza kuzigusia, lakini kulikuwa na changamoto za kimsingi ambazo ni za kisheria na ndiyo maana Mheshimiwa Waziri alipokwenda kule Mheshimiwa Simbachawene alichukua hatua aliyoichukua na kuweza kusimamisha uendeshaji wa hoteli ile.
Mheshimiwa Spika, lakini ametoa maoni ambayo nayapokea na hivyo ndivyo ambayo tunafanya hivi sasa kufanya mawasiliano kati ya Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya TAMISEMI. Mawaziri wawili hawa wanaendelea kulijadili na kulitazama ili hifadhi za malikale ziweze kutumika kwa mujibu wa sheria inayotakiwa, lakini pia shughuli za utalii zifanyike kwa mujibu wa sheria tulizojiwekea.
MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Waswahili wana msemo kwamba ukitaka kujua utamu wa ngoma uingie ucheze. Tatizo hili ni kubwa sana na binafsi nilikwishaongea na Naibu Waziri akawa ameniahidi atanipelekea mtaalam kutoka Arusha, hili siyo tatizo la mwaka huu nashangaa jibu linasema kwamba wanaanza kufanya utafiti. Wale wanyama wanaendelea kuzaliana, wanaendelea kuleta usumbufu, sasa hivi wanaingia hata ndani wanaepua chakula kikiwa jikoni na ni hatari sana kwa akina mama na nikisema ni hatari kwa akina mama nadhani kila mtu anaelewa. Sasa nataka nijue huu utafiti utakwisha lini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, miaka ya nyuma nyani hawa walikuwa wanadhibitiwa na wananchi wenyewe kwa kuwaua kwa risasi ambazo zilikuwa zinagawiwa kutoka kwenye Ofisi ya Maliasili lakini sasa hivi wamekatazwa kufanya hivyo na Maliasili hawa hawa. Sasa naomba niulize Wizara, kwa kuwa imetamka kwamba inakusudia kuwashirikisha wananchi kwa kutumia silaha za jadi, je, Wizara iko tayari wananchi wenye silaha kama magobole na kadhalika watumie risasi kama utaratibu wa zamani?Mimi Mbunge wao niko tayari kuwanunulia risasi ili tupambane na hawa wanyama vinginevyo watuletee Wa-Congoman waje wawale kule na siyo kutuambia utafiti wakati wanaharibu watu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwanza Wizara kwa niaba ya Serikali inawapa pole wananchi wa maeneo ya kata zilizotajwa kutokana na usumbufu huo wa wanyama hawa nyani na ngedere na uharibifu wanaosababisha kwenye mashamba yao. Kwenye swali lake la kwanza la nyongeza anauliza utafiti utaisha lini, kwenye jibu la msingi nimesema utafiti huo unakamilika mwezi Disemba, 2017.
Mheshimiwa Spika, lakini kwa nini tunafanya utafiti wakati ni dhahiri kwamba wanyama wapo na wanasumbua na wanaharibu. Mimi nafikiri utafiti ndiyo njia nzuri ya kuweza kufika mahali kupata jibu au suluhisho. Ni sawasawa na mtu anayeumwa malaria ambaye hataki damu itolewe iende kwanza ikapimwe, nafikiri hiyo haitakuwa njia sahihi. Nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tumedhamiria na tunakusudia na mimi na wewe tunaweza tukapata nafasi kabisa kupeana taarifa ya mara kwa mara katika kipindi hiki kabla ya hiyo Disemba ili tuweze kuona tunasonga mbele namna gani.
Mheshimiwa Spika, kuhusu matumizi ya silaha, matumizi haya yapo kwa mujibu wa sheria na kama ni matumizi ya risasi za moto sheria zinakuwa kali zaidi. Katika eneo hilo hao Serikali inashughulikia masuala hayo kwa kushirikisha Wizara zaidi ya moja, si suala la Wizara ya Maliasili na Utalii tu.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi ni kwamba utafiti sasa ndiyo unaweza ukatuwezesha tuone ukubwa wa tatizo, uzito wake, kama utaainisha kwamba matumizi ya silaha za moto ni lazima basi labda tunaweza tukaenda huko kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo lakini kama kwenye utafiti tukiona tunaweza kutumia njia nyingine ambayo siyo silaha za moto basi itakuwa ni vema tutumie njia hizo ambazo tutazipata.
MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, huo mpango unaoandaliwa ni jambo jema na kwa kuwa mpango huo utatusaidia vijiji vinavyozunguka maeneo hayo kupata asilimia 26, ni lini maandalizi ya mpango huo yatakamilika? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa katika kata hiyo ulipo Msitu wa Minziro kuna kitongoji kinaitwa Bulembe na kwa kuwa katika kijiji hicho kuna ngome zilizotumiwa na Wajerumani kupigana Vita ya Pili ya Dunia na kwa kuwa katika eneo hilo huwezi kwenda kwa sababu hakuna barabara isipokuwa uwe jasiri kutumia pikipiki au kutembea kwa miguu zaidi ya saa sita, je, Waziri au Naibu Waziri yuko tayari kuandamana nami kutembea zaidi ya saa sita kwenda kuona vivutio hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa umesema kwa ufupi ni kwa ufupi kwa sababu na maswali yenyewe yalikuwa yanaelekeza kupata majibu kwa ufupi. Kuhusu swali lake la kwanza, lini mpango utakamilika, mpango huu utakamilika ndani ya mwaka wa fedha uliokwishaanza.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, je, Waziri au Naibu Waziri yuko tayari kuandamana naye kwenda kuona vivutio alivyovitaja ambavyo viko ndani ya msitu lakini pia ni vivutio vya malikale.
Mheshimiwa Spika, jibu lake ni kwamba mimi au Mheshimiwa Waziri wakati wowote ule tutakapokuwa tumepata fursa na hasa baada ya kikao hiki cha Bunge tutakuwa tayari kwenda kuona na tutaweza kuona namna gani tunaweza tukaondoa changamoto hiyo ya miundombinu ambayo ni mojawapo ya changamoto zinazosumbua kwenye sekta ya utalii.
MHE. DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza niishukuru Serikali kwa mchakato ambao unaendelea katika maeneo yale.
Swali la kwanza, kupitia huo Mradi wa KILORWEMP, wadau tulikaa mwezi Oktoba, 2016 katika Mji Mdogo wa Mikumi. Tulichokubaliana ni kwamba urejeshaji upya wa mipaka ile utazingatia ushirikishi wa wananchi. Serikali wamefanya hilo lakini changamoto hapa, tunapojadiliana, tunapokubaliana katika urekebishaji wa ile mipaka lakini wakienda site watumishi/wataalam wale wa Serikali wanagoma, wanaelekeza kuweka mipaka kama wanavyotaka wao. Kwa mazingira hayo bado wataendeleza mgogoro. Kwa nini sasa makubaliano yale na wananchi na wadau kwenye kijiji hayatekelezwi wanapokwenda kuweka upya ile mipaka? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali sasa mnafanya zoezi la kuondoa mifugo kwenye hifadhi kwa maeneo yale ya lile Bonde la Ardhi Oevu la Kilombero. Mifugo ile itakapotoka kule inakuja kwenye ardhi ya vijiji, ardhi ya vijiji ndiyo yenye vyanzo vya maji katika bonde lile la Kilombero. Je, Serikali mnavisaidiaje vijiji hivi kukabiliana na msukosuko huo wa ile mifugo itakapotoka kule kwenye lile bonde kuja kwenye ardhi ya vijiji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: MheshimiwaSpika, swali lake la kwanza linasisitiza juu ya umuhimu wa ushirikishwaji wa wananchi jambo ambalo kwenye majibu yangu ya msingi nimelifafanua kirefu kwamba kwa mujibu wa mipango ya Serikali ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kufanya uhifadhi uweze kuwa endelevu na kuweza kutimiza masharti ya sheria, kanuni na taratibu bado utekelezaji wake unaendelea kusisitizwa na kwamba Serikali itaendelea kuona umuhimu wa ushirikishwaji wa wananchi. Katika mradi huu wa KILORWEMP tayari tunao mpango huishi unaoitwa intergrated management plan ambao kwa mujibu wa Kanuni za Mkataba za RAMSAR Convention tunapaswa kuuzingatia.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nipokee maelezo yake ambayo nayasikia kwa mara ya kwanza hapa kwamba makubaliano yanayofikiwa katika vikao mbalimbali vilevile vya ushirikishwaji wa wananchi wakati wa kwenda kuyatekeleza kule site yanakuwa yana kasoro au yana upungufu. Hili naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa niaba ya Serikali tunalipokea ili tuweze kufika kule kwenye maeneo yanayohusika tuweze kuona pengine katika utekelezaji, utendaji unakuwa una kasoro. Kwa hiyo, tukifika kule tutakwenda kushirikiana kuona namna gani tunaweza kuondoa hizo kasoro ndogo ndogo zinazoweza kukwamisha dhamira kuu ya Serikali ya kuweza kufanya uhifadhi uwe na mafanikio.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la pili linalohusiana na uondoaji wa mifugo kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na changamoto zake, anataka kujua kwamba uondoaji wa mifugo katika maeneo yaliyohifadhiwa na mahsusi katika suala hili ni suala la Bonde la Mto Kilombero kwamba mifugo ile hasa ng’ombe wanapokwenda katika maeneo ya vijiji wanakwenda kusababisha changamoto nyingine ambazo na zenyewe zinakuwa ni kubwa vilevile pengine ni kubwa zaidi kuliko wanapokuwa wako kwenye hifadhi kwa mujibu wa maelezo yake.
Napenda nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba na hili nalo ni suala vilevile la ushirikishaji wa pande zote mbili kwamba Serikali na wananchi kwa pamoja tunapaswa kufanya kazi hizi kwa pamoja kwa kushirikishana ili kila mmoja atambue umuhimu wa uhifadhi lakini katika kusimamia uhifadhi, changamoto tunazokutana nazo wakati wa kusimamia tuweze kuzitatua kwa pamoja. Kwa hiyo, katika safari hiyohiyo ninayosema tutakuja tuweze kuona nini kiko site, tutaweza kuliangalia tatizo hili la mifugo inayoondoka katika maeneo ya hifadhi ya Mto Kilombero ili tuweze kuona namna ya kutatua changamoto hizo katika maeneo ya vijiji wanamoishi wananchi.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kuna mgogoro wa Hifadhi ya Kazimzumbwi kati ya Ukonga na Kisarawe na nimshukuru Mheshimiwa wa Maliasili na Waziri wa Ardhi na Mheshimiwa Waziri Mkuu tulishakutana tukafanya mazungumzo na kulikuwa na kesi Mahakamani ambayo imekwisha. Sasa wataalam wale wa Maliasili wameenda Kazimzumbwi, wamevunja nyumba za watu, wanapiga watu, wanaharibu mali za watu katika eneo hilo. Swali langu, hawa Waheshimiwa Mawaziri wawili, wapo tayari twende pale Kazimzumbwi au hapahapa Dodoma nipo tayari kuwaita wale wahusika tukae pamoja tukubaliane kumaliza mgogoro ule ili usilete maafa katika aneo lile? Ni hilo tu.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, swali lake linafanana na maswali yaliyoulizwa na muuliza swali la msingi hapo awali, ni changamoto za utekelezaji wa usimamizi wa maeneo yaliyohifadhiwa kwamba wananchi wamekuwa wakilalamika juu ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali zinazohakikishia Serikali kwamba tunasimamia maeneo yaliyohifadhiwa.
Mheshimiwa Spika, changamoto moja inayojitokeza hapa ni kwamba, kwa sababu suala hili linahusisha pande mbili; upande mmoja ni Serikali ambayo inasimamia sheria, kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu yako masuala ambayo ni lazima yatekelezwe ili kuhakikisha kwamba uhifadhi unafanikiwa lakini upande wa pili ni wananchi ambao kwa maoni yao wanadhani katika kutekeleza shughuli mbalimbali za usimamizi wa hizo hifadhi upo utekelezaji ambao una kasoro kwa sababu unaleta athari kwa wananchi.
Mheshimiwa Spika, sasa hapa haiwezekani kupata uhalisia, ukweli na uhakika bila kwenda kwenye uhalisia wenyewe. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwa sababu ameuliza Mawaziri hao wanaweza kuongozana naye kwenda kuona hali ilivyo huko au wale wananchi labda kupitia viongozi wao kama wanaweza kupata fursa ya kuja Dodoma na kuweza kuonana na Waziri mwenye dhamana na Msaidizi wake wanaosimamia Maliasili.
Mheshimiwa Spika, labda niseme tu kwa kifupi kwamba hii ya pili itakuwa ni nyepesi zaidi kwa sababu ahadi zetu za kufika kwenye maeneo mbalimbali ambayo yana changamoto zinazohusiana na maliasili na utalii zinakuwa ni nyingi na muda unakuwa hautoshi. Kwa hiyo, kama hili la pili Mheshimiwa Mbunge anaweza kulitekeleza kwa urahisi zaidi ni jepesi zaidi. Hebu tupate viongozi kutoka huko, waje hapa na kile ambacho wanaona kwamba ni sahihi kwa upande wao halafu tutakuja hapa kuzungumza masuala haya kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu kwa sababu suala hili la Kazimzumbwi limeshawekwa vizuri kwa mujibu wa sheria lakini kama zipo changamoto basi ni utaratibu tu wa Serikali sikivu kuweza kusikiliza wananchi wanasema nini.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge hebu fanya utaratibu wa kuweza kupata viongozi wanaotoka kwenye maeneo haya wakija hapa basi mimi na Mheshimiwa Waziri tutaweza kuona namna bora zaidi ya kuweza kuwasikiliza halafu tutaweza kuona namna ya kuweza kushughulikia matatizo yao kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza kwa Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, mwaka jana mwezi Julai tulikwenda na Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA kutembelea vyanzo vya maji kutoka Milima ya Shengena ambayo inatiririsha maji mengi ambapo yanapita siyo mbali sana na hifadhi hii ya Mkomazi kwa upande wa Same Mashariki. Naye akaridhia kwamba kweli yale maji yangeweza kuchukuliwa na kusaidia sana ambapo yatakuwa ni maji ya kudumu kuliko haya mabwawa ambayo yanakauka mara kwa mara. Sasa nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, kitu gani kimefanya ule mpango usitekelezwe na badala yake wanakwenda tena kuchimba mabwawa wakati tumeshaona mabwawa kwanza ni hasara kubwa na pili maji yake yanakauka kila mara? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Waziri yuko tayari kutuma wataalam wake wakatembelee tena hii mito hasa Mto wa Hingilili ambao ndiyo unashusha maji mengi na kulinganisha na tathmini yake na kuchimba mabwawa ni ipi rahisi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza, anatoa taarifa juu ya ziara yake na Mtendaji Mkuu wa Mamlaka za Hifadhi za Taifa Nchini (TANAPA) kwenye Milima ya Shengena ambapo analiambia Bunge lako Tukufu kwamba waliweza kuona uwezekano kwamba eneo lile ni chanzo cha maji ambacho kingeaminika zaidi na kwa hiyo anataka kujua kwa nini Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii isingetumia chanzo kile badala ya vyanzo hivi ambavyo tumevieleza hapa vya kutumia maji kutoka ardhini.
Mheshimiwa Spika, masuala haya ambayo ni ya kisayansi msingi wake mkubwa ni utafiti na baada ya ziara anayoizungumzia, kilichofanyika ni kuangalia faida na hasara yaani cost benefit analysis na baadaye gharama za kuweza kutekeleza mradi ule wa kujenga miundombinu na kukusanya maji kutoka kwenye Milima ya Shengena na kuyafikisha kwenye maeneo yanayohitajika, katika hatua za awali, ilionekana kwamba gharama zake kwa sasa hivi hayawezi kuwa yanaweza kumudu kibajeti kuliko kujenga kisima au visima hivi tulivyovieleza hapa sasa hivi.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kuwa hicho ni chanzo ambacho ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kingeweza kuwa ni cha kuaminika na cha kudumu zaidi lakini kikwazo ni suala la uwezo wa kibajeti hatujafunga hilo dirisha. Hilo dirisha bado liko wazi lakini tusingeweza kukaa sasa kusubiri kufanya jambo kubwa na la gharama kubwa badala ya kufanya lile linalowezekana kwa sasa hivi.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge akubaliane na Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kwamba kwa sasa tutaendelea kutumia njia hii ya visima vifupi na visima virefu wakati tukiwa tunaangalia uwezo wa kibejati utakapokuwa umepanda basi tutatekeleza lile la pili.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kwa kweli linamezwa na swali la kwanza kwa sababu alitaka kujua kama tunaweza kutuma wataalam kwenda kuangalia ile mito ambayo iko kule na kuweza kuona kama inaweza kutumika kama vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Spika, jibu lake ni lilelile tu kwamba katika mito anayoitaja hata kama tukienda sasa hivi itakuwa ni suala la kulinganisha gharama na kwamba Wizara imeona hatua hizi zinazochukuliwa kwa sasa hivi ni za mpito ambazo zinaweza kushughulikiwa na uwezo wa kibajeti uliopo, lakini njia zile nyingine za kudumu zaidi za muda mrefu zitaangaliwa hapo baadaye baada ya uwezo wa kibajeti kuwa umepanda.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii niseme kwamba kwanza Serikali haitutendei haki sisi Wabunge. Neno italipa fedha au kifuta machozi pindi hela itakapopatikana haliwafurahishi Watanzania kwa tukio lililotokea la Watanzania kupoteza maisha yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, kadhia hii kwa Jimbo la Mbulu Mjini ina changamoto kadhaa ikiwemo ukosefu wa Askari Wanyamapori na pia ratiba isiyoonekana ya wenzetu wa TANAPA na jamii zinazopakana na mipaka ya hifadhi na makazi ya watu. Tukio hili la mwaka 2015 lilipoteza maisha ya wananchi saba, siyo watano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine niishukuru Serikali kwa sababu, Mheshimiwa Waziri ameleta tu majibu ambayo hajayafanyia kazi kwa sababu, hadi sasa muda mchache uliopita, kama miezi miwili, mitatu, Serikali tayari imetoa fidia kwa wahanga hao wapatao wanne, lakini wale wengine hawakupatiwa hata fidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu sasa, kwa kuwa tatizo hili linagusa maisha ya Watanzania, je, ni kiasi gani cha fidia au cha kifuta machozi kinatolewa kwa wale wote waliopoteza maisha yao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Kwa kuwa tatizo hili linavunja mahusiano kati ya wananchi na wenzetu wa TANAPA ama Serikali, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuandaa ratiba rasmi itakayowaunganisha wadau wa mpakani katika Tarafa yangu ya Daudi ili waweze kujadiliana matukio yanayotokea na hatimaye kudumisha uhusiano kati ya Shirika la TANAPA na wananchi wa Jimbo la Mbulu Mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kama alivyosema tayari Serikali imekwishaanza utaratibu wa kulipa bakaa au madeni ambayo yamekuwepo ya muda mrefu yanahusiana na kifuta jacho na kifuta machozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sana madeni haya yamekuwa hajalipwa, lakini napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwa ujumla kwamba Serikali katika awamu hii imeshalipa madeni yaliyokuwa yanafikia kiasi cha shilingi bilioni 2.1 na hata sasa kuwa yamebaki jumla ya shilingi takriban milioni 500 peke yake. Mbulu ni mojawapo kati ya Wilaya ambazo zimelipwa malipo hayo na jumla ya fedha kiasi cha shilingi milioni 7,100,000 zimelipwa kwa madhumuni hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maswali yake mawili ya nyongeza; la kwanza, anazungumzia ni kiasi gani cha fedha kilichobaki kwa ajili ya malipo kwa Halmshauri ya Wilaya ya Mbulu? Katika takwimu nilizonazo, nina takwimu za ujumla wa kiasi chote ambacho fedha zinadaiwa kwa Serikali, lakini mahususi kwa ajili ya Mbulu, ukiacha hiki nilichotaja, kilicholipwa tukionana mchana naweza kumpa taarifa juu ya kifuta jasho na kifuta machozi kilichobaki kwa ajili ya Wilaya ya Mbulu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la pili la kuweka ratiba na utaratibu wa kuweza kujadiliana, kuisharisha mahusiano zaidi baina ya TANAPA na wananchi wanaoishi katika maeneo yanayozunguka hifadhi, hili ni jambo jema na Serikali inalipokea. Tutakwenda kufanya hivyo na tutamshirikisha Mheshimiwa Mbunge ili kuona kwamba tunaimarisha zaidi mahusiano hayo kwa ajili ya uendelevu katika utaratibu mzima wa hifadhi.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali ndogo la nyongeza.
Kwa kuwa hicho kinachoitwa kifuta jasho au kifuta machozi kwa mujibu wa Sheria ya Wanyamapori, imekuwa hailipwi kwa wakati pale ambapo wananchi wakipata uharibu wa mazao yao hasa katika maeneo ambayo yanapakana na hifadhi:-
Je, ni kwa nini Serikali sasa isifikirie kuanzisha mfuko wa fidia ambao utachangiwa na hizi mamlaka zote kama TANAPA, Ngorongoro ili wananchi wawe wanaweza kutapata fidia yao kwa wakati bila kucheleweshwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna changamoto kubwa sana kuhusiana na malipo ya vifuta jacho na vifuta machozi. Ukweli ambao ni wa kudumu, hakuna namna ambayo tunaweza tukalifanya zoezi hili kwa namna endelevu kwamba madai yote yanahusiana na vifuta jasho na vifuta machozi yakalipwa kwa kile kinachoitwa kwa wakati hata kama tukianzisha mfuko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili namna pekee ya kuweza kuliweka vizuri, namna bora zaidi ni kuzuia zaidi kuweka kinga na kupunguza matukio ambayo yanasabisha ulipaji wa vifuta jasho na vifuta machozi. Ndiyo maana pale awali wakati najibu swali la nyongeza nilisema wazo la kushirikisha jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi ni wazo la msingi zaidi. Ili kuweza kuona ni namna gani tunaweza kufanya uhifadhi kwa namna ambayo tunaweza kupunguza matokeo yanayolazimisha sasa Serikali ilipe vifuta jasho na vifuta machozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima twende kwa utaratibu wa kuweka ushirikishi zaidi na kuanza kuangalia kwamba wananchi hawakai kwenye maeneo ambayo ni ya mapito ya wanyama hawakai kwenye maeneo ambayo ni ya mtawanyiko wa wanyama na kufanya shughuli za kilimo na ufugaji kwenye maeneo yale. Pale inapotokea kwamba wanyama wanahama kutoka kwenye maeneo yao, maeneo ambayo siyo yale ya mtawanyiko ya yale ya njia za mpito, basi tutakuwa tumepunguza kwa kiwango kikubwa matukio hayo, lakini pia tutaweka mbinu mbadala za kuweza kuzuia wanyama kuweza kuleta uharibifu kwenye mazao lakini pia kudhuru wananchi wanaozunguka maeneo hayo.
MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Pia katika Wilaya ya Karagwe kuna wahanga ambao wameathirika na wanyama waharibifu hasa tembo na viboko katika kata za Kihanga, Rugu, Nyakasimbi, Nyakabanga, Nyakakika na Bwelanyange, lakini pamoja na kushindwa kuwapa kifuta machozi wananchi hawa, pia vijiji katika hizi kata vinapakana na Pori la Akiba la Kimisi na Burigi na kuna asilimia ambayo inatakiwa kutoka kwenye mapato ya hifadhi kwenda kwenye vijiji ili kuwasaidia katika shughuli za maendeleo. Tumetuma madai katika Wizara kwa muda mrefu, lakini hatujawahi kupata hii fidia ili wananchi hawa nao wafaidike.
Je, ni lini Serikali itatoa kifuta machozi hicho pamoja na yale mapato? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nilisema katika maombi ambayo yameifikia Wizara kwa ajili ya uhakiki, kiwango cha jumla ya fedha takribani shilingi milioni 500 pekee ndicho ambacho kimebaki bila kulipwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda kuangalia kwenye orodha ile ya wale ambao wanafanya jumla ya madai yawe shilingi milioni 500 nione kama wananchi wanaolizungumzia ni sehemu ya madai hayo. Kwa hiyo, ikiwa hivyo ndivyo, tumesema fedha hizi zinalipwa ndani ya mwaka wa fedha huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa siyo miongoni mwa wale ambao jumla ya fedha shilingi milioni 500 zinadaiwa, basi itakuwa wako katika mchakato; wale ambao bado taratibu hazijakamilika kwenye ngazi za Halmashauri na Mikoa, kwa hiyo, tutakwenda kuhimiza tu ifanyike haraka ili madai hayo yaweze kuifikia Wizara yawekwe kwenye orodha halafu tuweke utaratibu wa ratiba ya kuweza kuyalipa.
MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri alipokuja kule Mufindi hakufika kwenye Jimbo la Mufindi Kusini kuzungumza na wananchi na ukizingatia Jimbo la Mufindi ndilo lililozungukwa na misitu sasa wananchi wanakuuliza, je, utaenda lini ili uweze kuongea na wale wadau wanaozunguka msitu ule? (Makofi)
Swali la pili, kuna makundi ya vijana wameshajiunda tayari ambao wazazi wao waliacha maeneo makubwa sana ambayo yalichukuliwa na watu wa Maliasili na vikundi hivyo Igowole kuna vijana 60, Mninga 60, Kihanga 60, Nzigi 60, Mtwango 60, Sawala 60, Kasanga 60, Mabaoni 60, Kitasengwa 60, Kiyowela 60, Nyororo 60, Kibao 60, Mkalala 60, Mbala Maziwa 60, Malangali 60, Mtambula 60, Ihowanza 60, Logolofu 60 na Luhunga 60. Hawa ni vijana waliojiunga kwenye vikundi tayari na ukitokea moto wanakimbia mbio na bodaboda kwenda kuzima moto katika msitu ule. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa viko vikundi 20 tu na wanaomba kila kikundi kipewe kibali kimoja, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari mgao huu kuwapatia vibali vyao vijana?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza kuhusu ziara ile niliyoifanya na maelezo kwamba baadhi ya maeneo ambayo yanapakana na shamba la Sao Hill sikuweza kufika. Kwanza ni kweli kutokana na ratiba niliweza kufika tu kwenye baadhi ya maeneo lakini nataka nimthibitishie kwamba bado umuhimu wa kutembelea kwenye maeneo yaliyobaki uko pale pale. Jitihada za Serikali za kuweza kutekeleza Ilani ya CCM, ya kuhakikisha kwamba Hifadhi za Taifa zikiwemo hifadhi za misitu zinawanufaisha wananchi wanaoishi jiraniau wanaopakana nazo iko pale pale na kwa hiyo, napenda tu nimhakikishie na nimpe ahadi tu kwamba nitafika kwenye maeneo hayo na safari hi sitafanya kikao pale Mufindi Mjini nitakwenda kufanya kikao kule kule mashambani porini niweze kuzungumza na wanavijiji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu vikundi alivyovitaja na idadi ya vijana ambao wako kwenye vikundi hivyo. Kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, nani vyema tukaenda kwa pamoja na Mheshimiwa Mbunge kwanza nikupe pongezi kwa kuwatetea na kuwazungumzia vijana hao na wananchi kwa ujumla katika maeneo hayo. Lakini vilevile niseme kwamba ni nia ya Serikali sasa kwamba hatutasubiri vijana wasubiri tu kunufaika na uvunaji wa mazao ya misitu kutoka kwenye misitu ya Taifa. Lakini sasa mwelekeo ni kuweza kuwafanya vijana na wenyewe waweze kumiliki mashamba yao ndio maana tunagawa mbegu kama vile ambavyo nimesema kwenye jibu la msingi miche karibu laki sita iligawiwa kwenye matukio ya pale awali.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendeleza utaratibu wa kuwezesha vikundi hivyo ili baadae viweze kusimama vyenyewe kwa kuwa na mashamba ya kwao ya miti. Nitoe wito na ushauri kwa Halmashauri inayohusika kuweza kuwagawia maeneo vijana hao ili waweze kupata miti, wachukue miche kutoka kwenye Wizara yangu na waweze kupanda katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maombi yake kwamba katika maombi ya mwaka huu kuweza kuzingatia maombi ya vijana wake kwenye eneo lile ninalichukua nitalifikisha kwa wataalam. Lakini litaenda kutazamwa sambamba na maombi mengine ambayo yamekwishapokelewa kwa mujibu wa muongozo ambayo nimeutaja hapo awali.
MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Kwa kuwa asilimia kubwa ya wanawake hapa Tanzania wako kwenye vikundi vya ujasiriamali hususani Mkoa wangu wa Iringa na changamoto kubwa ya hivi vikundi havina miradi endelevu ambayo ingekuwa msaada mkubwa sana kuwasaidia hawa akinamama kuendelea kupambana na hizi changamoto zao wanazopambana nazo kila siku.
Sasa Mheshimiwa Waziri huoni hii ni fursa kubwa pamoja na kazi nzuri ambayo mmewasaidia vijana. Huoni hii ni fursa nzuri sasa kuwasaidia akina mama wote sio tu wale wanaozunguka ule msitu bali akina mama wote wa Mkoa wa Iringa na Wilaya zote, Iringa Mjini, Iringa Vijijini, Kilolo na Mufindi ili waweze kunufaika na msitu huu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakubaliana naye kabisa na huo ndiyo mwelekeo wa Serikali kuongeza ajira miongoni mwa vijana, lakini pia kuongeza ajira miongoni mwa akina mama. Sasa misitu ni eneo moja ambalo Serikali inaweza kufikia malengo yake ya kuweza kufanya vijana na akina mama wakaweza kupata ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na mwelekeo wa Serikali nitoe wito kwa Halmashauri zinazohusika katika Mkoa wa Iringa, baada ya akina mama kuwa wamejiunga katika vikundi basi waweze kupewa maeneo, halafu baada ya pale kwa shughuli zile za kiutaalam na utoaji wa mbegu na pia hata usimamizi wa kutoa utaalam na kuhakikisha kwamba mashamba hayo yanastawi vizuri wataupata kutoka Wizarani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kuanzia sasa tuwe na mwelekeo wa kuhakikisha kwamba sekta ya misitu ichangie sana kwenye lengo la Serikali kuweza kutoa ajira za kutosha upande wa akina mama na kwa vijana.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Kwa kuwa Wilaya ya Lushoto ina misitu ya Shume Magamba na mingine midogo midogo na vijana walio wengi Lushoto hawana ajira, je, Serikali haioni sasaimefikia wakati wa kuwapatia vijana hao vibali ili na wao waweze kuwa na ajira?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi na kama nilivyojibu kwenye maswali ya nyongeza yaliyotangulia, ni kweli kwamba, kama Taifa sasa tunakwenda kuhakikisha kwamba tunapunguza kwa kiwango kikubwa na kwa kadri itakavyowezekana jinsi jitihada zinavyozidi kuendelea ni nia ya Serikali ikiwezekana kumaliza kabisa changamoto hii ya ajira nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, na nimesema kwamba Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia sekta zilizoko chini ya Wizara hii na sekta ya misitu ikiwa ni mojawapo tunaweza kutoa mchango mkubwa na ndio mwelekeo kwamba tunaenda kutoa mchango mkubwa wa kuweza kutoa ajira kwa ajili ya makundi mbalimbali nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kusubiri vibali kwa ajili ya kuvuna misitu ya Taifa haliwezi peke yake likawa ni suluhisho la ajira katika Taifa, isipokuwa kupitia vibali hivyo vidogo au vichache vikundi vinaweza vikapata mitaji. Lakini kutokana na vyanzo vingine vikundi hivyo baada ya kujiunga viweze kujenga uwezo wa kuwezesha kuweza kupata mikopo kutoka kwenye benki mbalimbali ili waweze kujiunga na kuweza kuanzisha mashamba yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mashamba yao wenyewe wataweza kuwa na misitu ambayo itakuwa ni mikubwa, lakini pia wataweza kutokana na biashara ya misitu hata wakaanzisha viwanda vidogo vidogo vya mbao (saw mills). Kama nilivyosema kwenye majibu ya msingi na baada ya pale ajira itakuwa ni ya uhakika kwa ajili ya wao wenyewe kwenye vikundi lakini pia wanaweza kuajiri hata wengine ambao watakuwa wako jirani nao.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Kumekuwa na uvunaji holela wa mikoko katika eneo la Rufiji na mikoko hii ikiwa inasafirishwa kwenda Zanzibar kwa kutumia bandari bubu. Je, Serikali inajua kuhusu suala hili na je, itachukua hatua gani?
Swali la pili, kumekuwa kuna uvunaji na utoaji holela wa mbao au mazao ya misitu katika maeneo ambayo hayana hata hiyo management plan au strategy ya uvunaji wa rasilimali hii. Je, Serikali ina mpango gani kupambana na hii hali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya maliasili na utalii kwa ujumla viko vitendo ambavyo kwa ujumla wake vinaitwa ujangili na ujangili hauishii kwa wanyamapori tu peke yake na bidhaa zao, ujangili pia unahusisha bidhaa za misitu na misitu yenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo vyote ambavyo vimekuwa vikifanyika vya ujangili ni kinyume cha sheria na Wizara au Serikali kwa ujumla imejipanga vizuri zaidi sasa hivi kuweza kudhibiti vitendo vyote vya ujangili kwa kuimarisha ulinzi kwenye maeneo yanayohusika, kuboresha vikosi vya askari na kuwawezesha askari kuwa na vitendea kazi bora zaidi katika kufuatilia vitendo vya ujangili na kuchukua hatua mara moja.
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.
Kwa miaka mingi sana hadi mwaka jana mwanzoni, wananchi waliruhusiwa kufanya shughuli za uvuvi ndani ya hifadhi pamoja na ufugaji nyuki. Lakini toka mwaka jana mwanzoni Serikali ilipiga marufuku na wananchi wakiingia kule wananyanyaswa sana ikiwa ni pamoja na kupigwa na wafanyakazi wa Idara ya Wanyamapori na Wahifadhi.
Je, ni lini Serikali itaruhusu wananchi, waendelee kufanya shughuli za uvuvi na ufugaji nyuki, kwa kuwa kwa kufanya hivyo, itajenga mahusiano mazuri kati ya Serikali na wananchi?
Swali la pili, sehemu kubwa ya hifadhi hiyo ya Moyowosi haina alama kwenye mipaka yake na kwa kuwa wananchi wanakuwa wakinyanyaswa sana kwa ajili ya kufanya shughuli zao ambazo walikuwa wamekwisharuhusiwa na Serikali, ni lini sasa Serikali itakuwa tayari kuweka alama hizo za mipaka? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza wakati Serikali imetoa ruhusa ya kufanya shughuli zile za uvuvi na ufugaji nyuki, ruhusa ile ilizingatia masharti ya kitaalam kwamba shughuli hizi za kibinadamu kwa kiwango hicho ambacho kiliruhusiwa kilikuwa hakiathiri shughuli za uhifadhi katika eneo linalohusika na kwamba utaratibu huo, utaendelea kutumika pale itakapoonekana kwamba kuna umuhimu wa kufanya hivyo kwa ushauri wa wataalam.
Hivyo basi, ningeweza kusema kwamba tutakwenda kuangalia eneo hili specifically sasa hivi, mahsusi lakini kwa kuwa nimeishatangulia kusema kwamba Serikali tayari inao mpango wa kushughulikia masuala haya kimkakati zaidi, basi nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute subira kidogo, twende tukayaangalie yote hayo kwa pamoja.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili ya swali lake, kuhusiana na kwamba eneo kubwa au sehemu kubwa haina alama, hii ni mojawapo ya changamoto ambayo inasumbua masuala ya uhifadhi kwenye maeneo yetu kwamba maeneo mengi alama zake ziko kwenye kumbukumbu za kitaalam, unazungumzia coordinates kwa mfano. Coordinates kwa mtumiaji wa kawaida mwanakijiji ambaye anapakana na eneo hilo si alama ya kutosha kuweza kumfanya mwananchi huyo aweze kutii Sheria vizuri zaidi.
Kwa hiyo, tunaposema tunakwenda kushughulikia kimkakati zaidi, ni pamoja na kwenda kuweka alama za kudumu lakini zinazoonekana vile vile. Lakini pia zitakazoshirikisha wananchi wanaoishi au jamii zinazoishi kwenye maeneo hayo, ili tukubaliane kwamba kuanzia hapo sasa huo ndio mpaka, na mpaka huo utakuwa unaonekana vizuri, na kila mmoja atalazimika kuuheshimu.
MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Tumekuwa tukiona mapori mengi ya hifadhi yakiingiliana na makazi ya watu katika jamii na mapori hayo yamekuwa yametengwa kwa muda mrefu sana.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kugawa mapori haya ya hifadhi yaliyotengwa kwa muda mrefu kwa wananchi, ili waweze kufanya shughuli za kijamii kama kilimo, na mifugo na hii itaweza kuwaondolea adha ya migogoro ya wafugaji na wakulima?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali inayo taarifa na inatambua kwamba iko kiu kubwa ya wananchi wanaoishi kwenye maeneo yanayopakana na hifadhi kwamba pengine wangechukua maeneo yale ili waweze kuyatumia katika shughuli zingine za kibinadamu, ikiwemo kilimo, ufugaji, pamoja na shughuli zingine. Lakini ni kweli pia sisi sote ni wananchi na nchi ni moja na kwamba sababu za kuifadhi maeneo hayo zilizingatia pia uhitaji wa mahitaji yetu ambayo ni ya kudumu ya muda mrefu zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu utaratibu ule, wa kuweza kuyatwaa maeneo haya na kuyatumia kama Hifadhi, yalikuwa ni maamuzi yetu sisi sote pamoja, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, tulishirikisha Vijiji, Wilaya pamoja na Mikoa ili kuweza kukubaliana kwamba maeneo hayo yahifadhiwe kwa sababu ambazo zina maslahi mapana zaidi, si kwa Taifa tu, lakini pia hata kwa wananchi ambao ni wa nchi nzima na sio wale wanaoishi kwenye maeneo yale tu pale walipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, narejea tena kusema kwamba kwa sababu umepita muda mrefu tangu maeneo hayo yalipotwaliwa kuwa kama hifadhi, pengine mazingira yamebadilika, pengine kuna sababu ambazo zinaweza zikaonekana kwamba zina uzito zaidi hivi sasa, ndio maana nimesema Serikali inakwenda kulishughulikia suala hili kimkakati, itakuwa ni pamoja na kushirikisha wananchi upya, wote twende tukaangalie na tupime kwamba je, sasa tuseme nchi hii isiwe na hifadhi kabisa? Maeneo yote tutwae kwa ajili ya shughuli zingine za kibinadamu? Pengine hiyo itakuwa ni upande mmoja haiwezekani.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tukisema kwamba kinyume chake kwamba maeneo yale ya hifadhi yote yabaki kama yalivyo, pengine kuna maeneo tunatakiwa kufanya marekebisho kidogo. Sasa tukatae kwa sababu kuna Sheria, hata kama kuna ukweli kwamba kwa sasa hivi kuna sababu za msingi, pengine na yenyewe itakuwa si sahihi. Ndio maana tunasema kwamba sasa Serikali pamoja na wananchi wanaoishi kwenye maeneo hayo, na pengine wananchi kwa nchi nzima wakitoa maoni tutakwenda kufika mahali sasa tukubaliane kwamba maeneno yapi tunahifadhi, kwa sababu zipi ambazo zitakuwa ni kwa maslahi ya taifa. Niwakumbushe sio kwa maslahi tu ya Taifa, sisi kama nchi tumesaini pia mikataba ya kimataifa, kuhusu masuala ya uhifadhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, muda hautoshi ningeweza kusema zaidi lakini napenda kuishia hapa, tunakwenda kufanya zoezi hili kwa pamoja, kutatua kero hizi kwa namna ambayo itakuwa ni endelevu, na ya kudumu.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niulize maswali mawwili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi wangu wa Kata za Kisiwani, Vumari na Mji Mdogo wa Same wamebanwa sana na Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi; na kwa kuwa Mwenyezi Mungu wakati anaumba dunia alimuumba binadamu akamwambia atawale viumbe vyote viishivyo kwenye maji na kwenye nchi kavu; na kwa kuwa wakati wa uhuru tulikuwa na idadi ya watu milioni 10.3 na sasa hivi tuko takribani milioni 50, tulikuwa na ng’ombe milioni nane sasa hivi milioni 28; tulikuwa na mbuzi milioni 4.4 sasa hivi ni milioni 16.6; tulikuwa na kondoo milioni tatu na sasa hivi ni milioni tano, tulikuwa na nguruwe 22,000 sasa hivi ni milioni mbili, astaghfilillah nimetaja nguruwe wakati ni mwezi wa Ramadhani, mnisamehe sana. (Kicheko)

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza je, Wizara ya Maliasili na Utalii iko tayari kushirikiana na Wizara ya Kilimo, TAMISEMI pamoja Ardhi ili waweze kutathmini eneo na idadi ya watu pamoja na mifugo wanayofuga ili kusudi kama kuna uwezekano maeneo ya hifadhi za misitu pamoja na Hifadhi za Wanyamapori zipunguzwe ili binadamu waweze kupata maeneo ya makazi pamoja na mifugo na kilimo?
Swali la pili, kwa kuwa Botswana, Afrika ya Kusini na Namibia wameweza kuzuia wanyamapori kutoka kwenye mapori kwenda kwa binadamu ama kwenye wanyama wanaofugwa, je, Serikali iko tayari sasa kuandaa mpango rasmi wa kuweka fence ili wanyamapori wasiweze kwenda kwenye makazi ya watu kuwasumbua na kuwaletea madhara ikiwa ni pamoja na vifo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali lake la kwanza Mheshimiwa Mbunge anazungumzia upungufu wa ardhi kwa ajili ya matumizi ya kibinadamu hasa kwa ajili ya faida ya kiuchumi na kijamii, akihusisha na uhaba au upungufu wa rasilimali ardhi kwa ajili ya shughuli hizo zinazotokana na ongezeko la binadamu na wanyama kama ambavyo amewataja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi Serikali inatambua na kwa kweli ni dhamira ya Serikali kuwafanya wananchi waweze kufanya kazi za kuzalisha mali kwa sababu ni kwa kufanya hivyo tu peke yake ndiyo hata madhumuni makubwa kabisa ya Serikali ya kuiondoa nchi kutoka katika uchumi wa chini kwenda uchumi wa kati yatafanikiwa, ni kwa kufanya kazi tu peke yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili wananchi waweze kufanya kazi lazima waweze kuwa na ardhi au wawe na maeneo ya kufanyia kazi. Kabla hatujaanza kusema kwamba maeneo tunayoyatumia hayatoshi ni lazima kwanza tuone maeneo hayao yanatumikaje hivi sasa, kwa hiyo, hapa ndipo ambapo tunazungumzia juu ya suala la mpango wa matumizi bora ya ardhi.
Kuhusu swali lake tutashirikiana vipi na Wizara nne zile alizozitaja ukweli ni kwamba Mheshimiwa Mbunge anafahamu kwamba tayari tunayo Kamati ya Kitaifa ya Wizara alizozitaja ambayo iko kazini inashughulikia suala hilo na baada ya utafiti wa kitaalam, baada ya kujiridhisha kitaalam tutapitia upya sheria na kuona katika kila eneo kama kweli suluhisho pekee la kuweza kuwafanya wananchi kupata eneo la kufanya shughuli za kibinadamu kama suluhisho pekee ni kugawa maeneo ambayo yamehifadhiwa kwa faida ambazo tunazifahamu ziko lukuki, basi Serikali itazingatia mwelekeo huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kutajitokeza ukweli kwamba bado maeneo tuliyonayo tunaweza kuyatumia vizuri zaidi bila kuathiri maeneo yaliyohifadhiwa basi hatutakuwa na haja ya kupunguza maeneo ya hifadhi isipokuwa tutajiimarisha zaidi katika kutumia vizuri zaidi maeneo ambayo hayajahifadhiwa kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili juu ya kuweka fence, kuweka uzio kwa ajili ya kuzuia wanyamapori kwenda kwenye maeneo ambayo ni ya binadamu, kwa ajili ya maeneo ya makazi ya binadamu na maeneo ambayo binadamu wanafanya shughuli za kibinadamu za kiuchumi na kijamii; napenda tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba huko ambako anazungumzia kwamba udhibiti umefanikiwa njia iliyotumika siyo hii tu peke yake ya kuweka fence, njia ya kuweka fence ni njia mojawapo na inatumika tu pale ambapo ni lazima kuweka fence kwa sababu njia hii ni ya gharama kubwa na si rafiki pia kwa mazingira hata kwa wanyama wenyewe na hata kwa binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kwa sasa hivi ni kwamba Serikali inalichukua suala hili na kwa kweli tumekuwa tukilifanyia kazi muda mrefu kuweza kuona ni namna gani tunaweza kudhibiti kiwango na kasi ya Wanyamapori kutoka kwenye maeneo yao na kwenda kwenye maeneo ambayo ni ya binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la msingi hapa vilevile na binadamu na wenyewe tusiendelee na utaratibu ule wa kwenda kukaa kwenye maeneo ambayo aidha ni njia za wanyapori au ni maeneo ya mtawanyiko ya wanyamapori.
MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la hifadhi ya Mlima Kilimanjaro una eneo la Half Mile au 0.8 ya kilometa, huduma za jamii kwa mfano uvunaji wa majani, uvunaji wa kuni kusafisha vyanzo vya asili vya maji, kwa mfano mifereji, inahusu vijiji 42 vya Halmashauri ya Wilaya ya Moshi. Wakati huu hakuna mahusiano mazuri kati ya wananchi wa vijiji hivi 42 pamoja na Hifadhi chini ya KINAPA hasa wale askari. Serikali haioni ni vema pande zote zinazohusika yaani wawakilishi wa vijiji pamoja na KINAPA ikisimamiwa na Serikali kuweka taratibu na kanuni endelevu zinazoaminika za mazingira ya kisasa ili mahusiano mema kati vijiji 42 na Hifadhi ya Mlima Kilimajora viweze vikawa vya mazingira ya kisasa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi kabisa Serikali inazingatia ukweli kwamba ili uhifadhi uwe endelevu ni sharti wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi husika, wanaopakana nazo waweze kuona kwamba wao ni sehemu ya huo uhifadhi kwenye hayo maeneo yanayohusika.
Kwa hiyo, njia zote zinazotumika katika kukamilisha malengo ya uhifadhi ni lazima ziwe rafiki kwa wananchi ambao wanazunguka kwenye maeneo hayo. Kwa sasa Serikali inachokifanya ni kuanzisha taratibu za kuwasogelea wananchi kwa ukaribu kabisa na kuwashirikisha, kuwapa elimu kwanza ya manufaa ya uhifadhi wenyewe, pia kuona namna gani wanaweza kushiriki kwenye jitihada za Serikali za kuhifadhi, muhimu zaidi mwishoni kabisa ni kuona namna ambavyo wananchi hawa wanaweza wakanufaika na uhifadhi moja kwa moja ukiacha ule utaratibu wa kunufaika na uhifadhi kwa njia na taratibu za kawaida za Kiserikali.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wakati anajibu suala la Mbuga ya Mkomazi na Mbuga ya Mkomazi kwa Mkoa wa Tanga kuna Wilaya ya Lushoto, Korogwe na Mkinga. Tatizo la mipaka hata kule linatuathiri na kuna timu sasa inapita kutathmini hilo tatizo, nataka nitambue, je, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili imeshirikiana na hawa watalaamu ambao wanapita kutathmini ile mipaka, hasa katika eneo la Mwakijembe Wilaya ya Mkinga?

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mbuga ya Mkomazi kwa Mkoa wa Tanga iko katika Wilaya za Lushoto, Korogwe na Mkinga na hili tatizo la mipaka sasa hivi kuna timu ya ambayo iko chini ya RAS kwa kule Tanga inafuatilia haya maeneo yenye migogoro ambayo wananchi na mbuga wanakinzana hasa eneo la Mwakijembe katika Halmashauri ya Mkinga, je, Wizara ya Maliasili na Utalii inatambua uwepo wa hii timu ambayo inakagua mipaka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa timu hiyo inayokagua mipaka.
Lakini Mheshimiwa Mbatia nafikiri wakati nikiwa namjibu swali alikuwa anasisitiza lini nilimuona wakati anataoka alikuwa anaendelea kuongea anauliza lini, sasa Mheshimiwa Mbatia tukimaliza kikao hiki cha Bunge (Kamati ya Fedha hivi) mimi na wewe tuambatane tukaangalie uhalisia ulivyo halafu tuweke ratiba ya kushughulikia suala hilo.
MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kuwa tunajua umuhimu wa misitu na miti na kazi zake katika jamii na katika ekolojia, ni vizuri tukajua kwamba afya ya miti au misitu yetu ikoje. Sasa kwa kuwa kuna changamoto ya kibajeti kwenye Idara hizi za Tafiti za Misitu, napenda kujua Wizara inajipangaje ili kuweza kuweka sawa tathmini ya hali ya misitu nchini in terms za afya?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kujua kwamba, Wizara inaweka mikakati gani madhubuti ili kuweza kuondokana na changamoto ya upotevu wa misitu kutokana na kukata miti ovyo au uvunaji holela wa miti? Sasa Serikali inajipangaje kujua ni aina gani ya miti na idadi ya miti inapangwa sehemu gani na inashirikishaje jamii ili zoezi hili liwe na manufaa na endelevu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la kwanza, Wizara imejipangaje katika kuangalia afya ya miti? Kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi, chini ya Taasisi ya TAFORI ambayo ni mahususi kabisa kwa ajili ya kufanya tafiti, Serikali inafuatilia hali ya misitu nchini kwa namna ambayo ni endelevu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wote tunaangalia misitu yetu inaendaje ili kuweza kubaini matatizo yanayoweza kutishia uharibifu wa misitu kutokana na magonjwa na changamoto nyingine zinazohusiana na afya ya miti kwa mfululizo ambao, kwa kuwa ni endelevu, changamoto zinazoonekana zinashughulikiwa mara tu zinapogundulika huko kwenye misitu yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inawezekana kupitia jitihada mbalimbali ambazo ni za Serikali kwa maana ya kupitia bajeti za ndani. Pia kwa sababu suala la uharibifu wa mazingira, masuala ya maendeleo endelevu; haya ni masuala yanayotazamwa na dunia nzima kwa pamoja kwa sababu uharibifu wa mazingira unaathiri dunia yote kwa pamoja. Kwa hiyo, kupitia taasisi mbalimbali ambazo zina maslahi katika kuhakikisha kwamba kuna maendeleo endelevu na utunzaji wa misitu unakuwepo, Taasisi hii ya TAFORI mara kwa mara kwa kupitia maombi mbalimbali inapata support ya kibajeti na kuweza kukamilisha majukumu hayo.
Meshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, napenda kusema kwamba tunao Mkakati wa Taifa wa Kupanda na Kutunza Miti. Hapo awali tumekuwa tukielekeza nguvu kwenye kupanda miti peke yake, lakini sasa baada ya kuona kwamba baada ya kupanda miti bila kufuatilia utunzaji wake na kuhakikisha kwamba inakua, tunapoteza asilimia kubwa sana ya miti ambayo tumetumia rasilimali nyingi sana katika kuipanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika mkakati huu wa Taifa wa sasa hivi unaopita katika kipindi cha miaka mitano ijayo, kuanzia mwaka 2016 mpaka mwaka 2020, Ofisi ya Makamu wa Rais ikiwa ndiyo inayoongoza, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Ofisi ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Asasi za Kiraia, Washirika wa Maendeleo pamoja na Sekta Binafsi, wote katika mkakati huu wamegawana majukumu ya kuhakikisha kwamba tunafanya jitihada za kufikia lengo hili ambalo nimelisema hapo awali la kuweza kufikia upandaji wa miti 1,075,000 kila mwaka katika muda wa miaka 17.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya muda mfupi misitu yetu itakuwa katika hali yake ya afya ya kawaida.
MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa nia ya Serikali ni kupanda miti nchi nzima ili kurudisha uoto wa asili uliopotea na vikundi vya Wilaya ya Lushoto vimeanza kutosha miche ya miti, hasa Kikundi cha Friends of Usambara. Je, Serikali itasaidiaje vikundi hivi, hasa hiki cha Friends of Usambara, maana mpaka sasa kimeshaotesha miche zaidi ya milioni tatu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Serikali inaunga mkono jitihada zote ambazo zinafanywa na mtu mmoja mmoja, lakini pia hata na vikundi. Hii ni taarifa njema ambayo Serikali inapokea kwa mikono miwili, uwepo wa vikundi katika eneo ambalo amelizungumzia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba awaelekeze wale wanakikundi waweze kuwasiliana na Wizara ili tuweze kuona namna gani Wizara inaweza kuwa-support.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Liwale ina misitu mikubwa miwili; kuna ule msitu ambao unahifadhiliwa na WMA (Ustawi wa Vijiji) na ule msitu wa Serikali ambao ni Msitu wa Nyera, Kipelele. Msitu huu ni msitu ambao tumeurithi kutoka enzi za Wakoloni, lakini mpaka leo harversting plan ya msitu ule haijatoka. Nini kauli ya Serikali kuharakisha harvesting plan ya msitu huu ili wananchi waweze kupata faida ya kuwepo kwa msitu huu wa Nyera, Kipelele? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika misitu miwili anayoizungumzia, labda niseme tu kwa ujumla, harvesting plan anayoizungumzia maana yake ni mpango wa uvunaji. Tunao mpango wa uvunaji ambao tumeupitisha hivi karibuni unaoeleza namna ambavyo tunaweza tukavuna misitu lakini tukizingatia uvunaji endelevu ili uvunaji usizidi kasi ya kukua kwa misitu na hatimaye tukajikuta kwamba tunamaliza misitu zaidi ya kuitunza na kuifanya iendelee kuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakati wowote ule Mheshimiwa Mbunge atakapopata nafasi aje Wizarani, tunaweza tukamwelekeza namna gani au tunaweza tukamwonesha harvesting plan jinsi ilivyo aweze ku-share na wananchi wa maeneo ambayo yanahusika kwa ajili ya matumizi ya wananchi wake.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, kwa kuwa kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri, uvunaji wa miti hata baada ya kukomaa unakatazwa; na kwa kuwa Jimbo la Same Mashariki hakuna hata vitalu vya miti. Je, ni namna gani Serikali itahakikisha kwamba kunaanzishwa vitalu ili wananchi waweze kupata miche ya kuweza kupanda kwenye maeneo yao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wengi walihamasishwa na walipanda miti mingi na wengi walichukua mikopo ili wapande miti kwa biashara, lakini inapofika wakati wa uvunaji wanahangaishwa sana na Halmashauri hata pale Wizara ilipotoa maagizo kwamba waruhusiwe kuuza miti yao. Je, Mheshimiwa Waziri anatoa tamko gani hasa kwa Halmashauri ya Same ili wajue kwamba Wizara ina msimamo gani juu ya suala la wananchi waliopanda miti yao waweze kuivuna na kuiuza kibiashara? Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kaboyoka katika swali lake la kwanza, anataka kujua ni namna gani Serikali itawawezesha wananchi wa kule Same Mashariki kuwa na vitalu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali lililotangulia, katika mkakati wa upandaji miti Kitaifa, kila Halmashauri ya Wilaya imepangiwa kupanda miti kwa wastani wa miti milioni mbili kila mwaka. Nasema ni wastani, kwa sababu itazingatia ukubwa wa Halmashauri, idadi ya watu, hali ya hewa ya Halmashauri inayohusika, kuona maeneo rafiki ambayo miti inaweza kupandwa. Kwa hiyo, ziko Halmashauri nyingine zitapanda miti zaidi ya hiyo, Halmashauri nyingine zinaweza zikapanda miti pungufu ya hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uwepo wa vitalu vya miti ni suala ambalo litafanyika baada ya kazi ya mkakati huu kuwa imefikia katika Halmashauri hiyo na kwa hiyo, mtaweza kupata ushauri kutoka Wizarani chini ya mkakati huo nilioutaja ili muweze kuoneshwa ni maeneo yapi, ya ukubwa gani muweze kuwa na vitalu vya kuweza kupanda miti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili la Mheshimiwa Kaboyoka, anataka tamko kuhusiana na miti ambayo inakatwa kwenye maeneo ambayo ni ya miti ya kupandwa ukilinganisha na hatua za udhibiti kwa mujibu wa sheria ambayo inazuia ukataji miti hovyo ambayo inaendana na uharibifu wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu nimshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba ni jukumu la Serikali sasa kuweza ku-balance na tunaposimamia ukataji wa miti kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo mkaa na matumizi mengine, hatutakataza matumizi ya miti halali ambayo imepandwa kwa njia halali, isipokuwa usimamizi wake unaendana na upataji wa vibali mahususi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Taasisi chini ya Wizara zilizoko katika Halmashauri hiyo zitaweza kutoa utaratibu ambao chini ya utaratibu huo miti halali iliyopandwa kwa madhumuni hayo ikiwa imekidhi vigezo vya kisayansi kama vile kukomaa na mambo mengine, utaratibu huo hauwezi kuzuiliwa.
Mheshimiwa Mbunge, ufafanuzi zaidi kuhusiana na suala hili unaweza ukapatikana wakati wowote ule baada ya session hii.
MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ni dhahiri mbinu zote za ulinzi zinazotumika pamoja na ulinzi shirikishi bado hazijasaidia kutatua tatizo la uharibifu wa misitu na hususan misitu ya asili kwenye nchi yetu. Je, Serikali inafikiria nini sasa kuhusu mbinu mbadala ya kuhakikisha kwamba misitu yetu inahifadhiwa na kuendelezwa kwa ajili ya kizazi kijacho?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza siyo jambo jema sana kuthibitisha hapa kwamba jitihada zote zile za kisheria na zile za kupitia ushirikishaji wa wananchi zimeshindikana kuweza kuzuia tatizo hili la uharibifu wa mazingira. Napenda kuungana na Mheshimiwa Mbunge kuona kwamba jitihada hizo bado zipo na zinatakiwa kuendelea. Tunatakiwa tu kuboresha namna ambayo tumekuwa tukifanya hapo nyuma, maisha bado yanaendelea ili tuweze kuhakikisha kwamba uhifadhi wa mazingira unaendelea kuwepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaongeza idadi ya Wataalam ili waweze kusimamia vizuri zaidi, lakini pia tutaweza kusimamia misitu ili tuweze kupunguza uharibifu wa mazingira.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa uwepo wa Msitu wa Shengena, Msitu wa Shangai na Msitu wa Bombo ndiyo unaosaidia uwepo wa Hifadhi ya Mkomazi; lakini katika Msitu huo wa Bombo kuna uvamizi mkubwa unaofanywa na wananchi. Je, ni lini sasa Serikali itaweka mipaka (beacons) kutenga eneo hili la Msitu wa Bombo ambao ni msitu maalum wa kuvuta mvua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kabisa msitu wa Bombo ni msitu muhimu sana kwa ajili ya Hifadhi ya Mkomazi, lakini pia kwa ajili ya ikolojia nzima ya eneo la Mkomazi. Sasa lini Serikali itaweka beacons?
Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la uwekaji wa beacons linaendelea nchi nzima na nataka nimhakikishie kwamba kama bado hatujafika Mkomazi, nitakwenda kuangalia ratiba na kuona lini tunafika huko ili niweze kumpa tarehe kabisa, lini tunaweka katika hifadhi hiyo. Kwa hiyo, tuonane baada ya hapa, tuweze kuona ni lini beacons zinawekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ni mpango wa Serikali ambao unaendelea sasa hivi kuweka beacons au kuweka alama za mipaka katika hifadhi zote nchini.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru nami kuweza kupata muda wa kuuliza swali moja la nyongeza. Mamlaka ya Wanyamapori maeneo ya Ngwala, Itiziro na kule Guwa wamevamia vijiji hivyo na hivyo wamewasambaza wananchi, wamewanyang’anya mashamba, wamenyang’anya mbao na mali zao nyingine; na Mheshimiwa Naibu Waziri nilikwambia. Sasa nataka Mheshimiwa Naibu Waziri anithibitishie humu ndani mbele ya Bunge kwamba ni lini tutaongozana mimi na yeye twende tuka-solve mgogoro huo kwa ajili ya wanyamapori maeneo ya Ngwala?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi kama ulivyoelekeza, ni kwamba kwanza mpaka unahusisha pande mbili na ni vigumu sana upande mmoja kusema mwingine amemwingilia mwingine kwenye mpaka wake. Nafikiri njia sahihi, wote wawili wanaweza wakawa mahali pamoja halafu kila mmoja akaangalia vigezo nani ameingia kwa mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake, lini tutaweza kwenda; nilimwambia kabla na narudia tena kusisitiza, tukimaliza Bunge hili la Bajeti mimi na yeye tutapanga ratiba ambayo itakuwa ni rafiki, twende kwenye maeneo hayo, halafu tutaangalie namna gani tunaweza kutatua tatizo hilo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Jimbo la Mbulu Mjini mipaka yake kwa asilimia 50 inazungukwa na misitu ya asili na maji wanayotumia viumbe wakiwemo binadamu yanatoka katika misitu hiyo. Hivi sasa maji hayo yameanza kupungua ndani ya misitu. Je, ni lini Serikali itapeleka wataalam watakaofanya utafiti katika misitu inayozunguka Jimbo la Mbulu Mjini ili iweze kufanyia kazi taarifa yake ya utafiti kwa ajili ya kushauri jamii inayozunguka misitu hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka kusema tu Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba ameshafika Ofisini kwangu siyo mara moja na suala hili tumelizungumza, tumeliweka wazi, tumesema kwamba nina maslahi kwa wananchi wa Jimbo lile. Kwa hiyo, ni lini tunaenda? Jibu ni lile lile ambalo nilisema kabla; nimemwambia Ofisini na narudia tena hapa kwamba mara baada ya Bunge hili la bajeti, nina ziara ndefu sana, ratiba hiyo inahusisha pia Jimbo lake. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mheshimiwa Waziri anasema kwamba mpango mkakati mmojawapo ni kutangaza kuingiza hiyo tovuti na filamu. Hapa swali lilikuwa linataka kujua mkakati thabiti wenye dhamira ya kweli kwa sababu hapo wanaposema, hata barabara ya kufika kwenye hivyo vivutio hakuna. Sasa huu mkakati, hata hao watu unaoingiza kwenye filamu, watafikaje kule Kilwa ambapo kwenye hivi vivutio hamna barabara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba Pwani ya Afrika Mashariki ni mahali ambapo kwanza walikuwa na currency yao, yaani walikuwa na pesa yao; ni Kilwa, lakini haya yote watu hawayajui.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kwa mfano, ukiangalia Vita ya Majimaji; asili ya vita hii ni Kilwa, lakini makumbusho ya Vita ya Majimaji yako Songea. Sasa Wananchi wa Kilwa walitaka waone, Serikali inafanya taratibu gani kuirudisha Vita ya Majimaji Kilwa na kuitangaza Kilwa kama sehemu ya Utalii? Hilo ni swali la kwanza. (Kicheko)
Swali la pili...
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mheshimiwa Kuchauka nafikiri wewe na mimi kwa pamoja tunafahamu kwamba historia ya kwamba Kilwa haifikiki au haipitiki ilikuwa labda zamani; lakini kwa sasa hivi ninavyofahamu na nafikiri Wabunge wengi wanafahamu, kama unazungumzia barabara ya kufika mpaka Kilwa; ni ya lami, kwa maana vivutio vya Mjini Kilwa, yale magofu pamoja na maeneo mengine ya utalii wa kiutamaduni pamoja na utamaduni wa kihistoria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama anazungumzia Mbuga ya Selous, kufika ndani ya Hifadhi ya Selous, ni kweli kuna namna na haja ya kuboresha miundombinu ya kufika ndani ya Selous na kuzunguka ndani ya Selous yenyewe kwa maana ya barabara; lakini iko miundombinu ambayo ni maeneo ya malazi au facilities za malazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, upande mmoja ni jukumu la Serikali, kwa mfano kama barabara, lakini upande mwingine ni jukumu la taasisi binafsi ambazo sasa Mheshimiwa Mbunge usaidie Serikali mnapokaa kwenye Mabaraza kule ya Halmashauri kuweza kuona namna ambavyo mnaweza mkashirikiana na Serikali kuweza kuhamisha wawekezaji wakaweza kuweka vivutio ndani ya Selous.
Mheshimiwa Naibu Spika, pengine nimtaarifu tu Mheshimiwa Kuchauka kwamba mkakati anaoutaka mahususi sasa kwa ajili ya Kilwa yenyewe; sasa hivi tunakamilisha hadidu za rejea kwa ajili ya mkakati mahususi kabisa kwa ajili ya Kilwa. Siyo Kilwa peke yake, kwa ajili ya southern circuit. Huu ni utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Miaka Mitano ambao tunaposema kutekeleza Mpango wa Miaka Mitano, maana yake tunazungumzia diversification kwamba kutanua wigo wa vivutio vya utalii nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kupitia mkakati huo, tuna uhakika kwamba tunakwenda kuboresha mazingira ambayo yataboresha utalii ndani ya Selous lakini pia vivutio ambavyo viko Kilwa Mjini hasa vya utamaduni na kihistoria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Vita ya Majimaji, hilo suala bado linajadiliwa. Wako upande mmoja katika Kambi nyingine wanasema ni muhimu zaidi kuzingatia kwamba historia ya Majimaji ina mizizi zaidi Kilwa, wengine wanasema ina mizizi zaidi Songea. Sasa nafikiri unatingisha kichwa kwa sababu hayo ni maoni yako, lakini nafikiri suala hili linajadilika, lakini hali ilivyo kwa sasa hivi, mazingira yaliyoko sasa hivi yanazingatiwa kwa mujibu wa historia hiyo hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri utakumbuka siku za nyuma tulikaa hapa tukawa tunazungumzia kuhusu suala la historia kwamba wengine wanasema historia inabidi ziandikwe upya, lakini hatuna sababu ya kuandika upya, lakini tutaweza kuweka utaratibu ulio makini kuweza kuweka suala hilo likakaa sawa.
MHE. EDWIN M. SANNDA: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Spika, kwa fursa. Wilaya ya Kondoa hususan pale Kata ya Kolo na nyinginezo, ipo michoro ya mapangoni ambayo ni vivutio vikubwa sana vya kihistoria kwa ajili ya utalii, lakini vimekuwa havitangazwi sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuvitangaza ili kizazi cha sasa na cha baadaye kitambue hii fursa na kuweza kuitumia ili hatimaye pia kipato kiongezeke?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, michoro ya kwenye mapango ya Kondoa ni mojawapo kati ya maeneo ya utalii wa kiutamaduni na utalii wa kihistoria ambao tayari unafahamika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ambayo imebaki sasa hivi ni ya kuweza kuboresha matangazo kwa maana ya utangazaji wa utalii; na nimesema katika majibu yangu ya maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Kuchauka, kwamba tunachokifanya sasa hivi ni utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao unasisitiza juu ya diversification of tourist attractions, kwamba tunataka kuendelea kuboresha na kutanua wigo wa vivutio vya utalii ili tuondokane na vivutio vya utalii vinavyohusiana na wanyamapori peke yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, chini ya mpango huu, chini ya utekelezaji wa Mpango wa Miaka Mitano, tunakwenda kutangaza zaidi vivutio ambavyo ni vipya; vimekuwepo lakini vimekuwa havitiliwi mkazo, lakini sasa tunakwenda kuvitilia mkazo kwa maana ya kwamba tutaboresha zaidi matangazo kwa ajili ya vivutio vya aina hiyo.
MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kule Moshi Vijijini kuna vyanzo vingi vya kitalii ambazo havijatangazwa vizuri. Kwa mfano, kule Kata ya Uru Mashariki kuna maanguko ya maji ya ajabu sana yanaitwa Mnambeni na hivi karibuni katika Kata ya Mbokomu, kumevumbuliwa mti ambao unasemekana ni mrefu kuliko miti yote katika Bara la Afrika. Sasa nataka kufahamu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itachukua hatua za makusudi kuweza kuvitambua hivi vyanzo na kuvitangaza inavyostahili ili tuweze kuvitumia kikamilifu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu hii ni tajiri sana ya vivutio vya utalii. Kama nafasi ingekuwepo, karibu kila Mbunge hapa angeweza kusimama na kueleza kwamba katika Halmashauri yake kuna kivutio hiki na kile; sasa suala la kuboresha utangazaji siyo suala la Serikali peke yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali inaendelea na utaratibu wa kuweza kuboresha matangaza ambayo sasa hivi tunafanya, nitoe wito sasa kwa Mbunge moja moja lakini kupitia Halmashauri zinazohusika kuanza kuvibainisha vivutio vilivyopo kwenye maeneo yao ili viweze kwenda mbele ya wataalam wa Idara ya Utalii katika Wizara ya Maliasili na Utalii tuweze kuviorodhesha kwa pamoja, halafu tukubaliane kama vinakidhi viwango vya Kimataifa kama vivutio, tuweze kuvifanyia grading, halafu baada ya pale tuendelee na utaratibu wa kutangaza tukitambua kwamba ni jukumu letu sote.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 mwananchi mmoja wa Kenya alitamka maneno kwenye mkutano mmoja wa Kimataifa kwenye nchi mojawapo nje kule, kwa kurusha tu clip ndogo tu lakini ikatingisha dunia, lakini pia na sisi Watanzania tukaanza kusema kwa nini wanataka kuteka vivutio vyetu? Ule haukuwa mpango wa Serikali, ni mtu mmoja tu alifanya vile.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wananchi wa Tanzania nasi kwanza tushiriki katika utalii wa ndani ili tuvifahamu vivutio vyetu na sifa zake halafu baada ya pale nasi tuweze kushiriki kama Watanzania kutangaza vivutio vyetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza kushirikiana na wenzetu walioko nchi za nje kwa utaratibu wa diaspora ili tuweze kufanya nchi yetu ikapata kutangazwa sawa sawa kwa maana ya vivutio vya utalii. (Makofi
MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kule Wilayani Mbinga yako mawe mawili makubwa ya ajabu ambayo yanafahamika kwa jina la Mawe ya Mbuji; mawe haya yanasadikika kuwa ni jiwe la kike na la kiume; lakini pia katika mawe hayo viko viumbe hai vyenye kimo kifupi sana vinavyofanana na binadamu, viumbe hivi huwa vinajitokeza hasa msimu wa michezo ya utamaduni. Je, ni lini Serikali itafanya utafiti ili kubaini ni viumbe vya aina gani hivyo ambavyo vinaishi katika mawe hayo na hatimaye kutangaza eneo hilo kama eneo la utalii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye maswali ya nyongeza yaliyotangulia, nimesema nchi hii ni tajiri sana ya vivutio vya utalii, jambo ambalo hatujalikamilisha bado na tunaendelea kulifanya ni kuwa na orodha ya vivutio hivyo vilivyohakikiwa kwa sababu siyo kila kitu ambacho mtu mmoja anaweza kukiona kwamba kinatosheleza kuwa kivutio cha utalii, kinakuwa hivyo; ni mpaka wataalam wanaohusika waseme kwamba sasa hiki kinakidhi viwango vya Kimataifa vya kuwa kivutio cha utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii, tayari imeshawasiliana na Halmashari zote nchini ili kuweza kuviorodhesha vivutio hivyo, vifike Wizarani, tuvifanyie uchambuzi halafu tuweze kuviweka katika makundi (grading) halafu tuweze kuweka mkakati wa pamoja wa namna gani ya kutangaza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema jukumu la kutangaza lisiwe jukumu la Serikali peke yake; kama mnavyofahamu na mnavyoona, dunia ya sasa ni kama kijiji; na kila mmoja akitumia wajibu wake wa kutumia mifumo ya mawasiliano ya kisasa, tunaweza kutangaza nchi yetu kwa namna ambayo ni ya mafanikio zaidi.
MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa nchi yetu ina maeneo mengi ya masalia ya Wafalme pamoja na majengo; kwa mfano, Mtemi Shomali Mwanansali wa Igurubi, kuna majengo ya Mtemi Humbi Ziyota Mwanantinginya pale Ziba. Kwa nini Serikali sasa isiyatambue maeneo haya yote yenye majengo na masalia ya Watemi nchini kote na kuyatangaza? Najua wenzetu kutoka Ulaya watakuja kuyaangalia. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo yalikuwa makazi au hata ni makazi hata sasa ya viongozi wetu wa kimila; Watemi, Mamwinyi na wengineo, kweli ni maeneo ambayo licha ya kwamba ni ya kihistoria, yana vivutio kwa sababu kimsingi yana record ambayo inaweza kutupa hata mafundisho kwa ajili ya siku za usoni. Kama ambavyo tunajua historia na faida zake, kwamba unaangalia tulikotoka, hapa tuliko na huko mbele tuendako, inaweza kuwa ni mchango mkubwa sana kwa upande wa maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza tukajiuliza, hivi ni kwa kiasi gani sisi wenyewe kwanza tunatembelea maeneo hayo? Ni kwa kiasi gani sisi wenyewe tunayapenda maeneo hayo na tunayatunza kabla hatujafikiria hata kuyatangaza kwa ajili ya watalii kutoka nje? Sasa wito nilioutoa kabla na napenda kuurudia tena hapa, tuanze sisi wenyewe kwanza kwenye Halmashauri zetu kuanza kuthamini maeneo hayo, kuyaweka vizuri katika ubora wake, halafu baada ya pale, kuwasiliana na Wizara ya Maliasili na Utalii na kuweza kuona namna gani tunaweza kuviboresha na kuvitangaza vivutio hivyo ndani na nje.
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana nami kupata fursa hii ya mwisho ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa mazingira ya kusini katika maana ya Ruaha, Rufiji mpaka Kilwa yanafanana kabisa na Hifadhi ya Msitu wa Liparamba unaounganisha upande wa Nyasa, Mbinga Mjini na upande wa Msumbiji. Ni lini Hifadhi ya Liparamba itapata hadhi inayostahili ili iwe kivutio cha utalii kwa center ya Kusini, hususan tunaunganisha nchi mbili za Msumbiji na nchi ya Malawi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli kwamba Hifadhi ya Liparamba iliyopo mkoani Ruvuma ni mojawapo kati ya maeneo ya hifadhi ya wanyamapori machache sana kwa Mkoa wa Ruvuma, lakini tajiri kwa wanyamapori na ambayo inastahili kabisa kuwa kwenye viwango vya Kimataifa vya kuwa mojawapo ya maeneo yenye vivutio vya utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli pia kwamba katika siku za nyuma, mkazo wa kuweka mipango na mikakati ya kuweza kuboresha utalii katika hifadhi hiyo, hapo nyuma hakukuwa na mipango madhubuti kwa sababu hatukuwa na utaratibu wa kuweza kuboresha utalii upande wa kusini mwa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hapo awali kwamba katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, tumezungumzia juu ya ku-diversify au kuweka utaratibu wa kuwa na mtawanyiko wa vivutio kwa maana ya vivutio vyenyewe; aina za vivutio, pia mahali vivutio vilipo hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, chini ya mpango huo, tutakwenda kuboresha utalii kusini na Hifadhi ya Liparamba ni mojawapo kati ya hifadhi ambazo zinaenda kuwekwa katika kipaumbele ili kuhakikisha kwamba sasa watalii hawaendi tu Arusha, Moshi, Kilimanjaro na maeneo ya Kaskazini, pia waweze kwenda Mbeya, Songea, Mtwara na maeneo mengine ya Kusini.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge atupe nafasi tuweze kukamilisha mipango iliyopo kwa ajili ya kutekeleza sehemu ya mpango wa miaka mitano ili tuweze kuona sasa tunaboresha utalii upande wa kusini.
MHE. HAMIDU H. BOBALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nimuulize maswali mawili ya nyongeza Mheshimiwa Naibu Waziri:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa lugha yoyote ambayo tunaweza tukazungumza haiondoi ukweli kwamba dinosaurian huyu ni mali yetu sisi Watanzania, kwa hiyo, manufaa yoyote yanapaswa sisi tuanze kunufaika. Sasa kwa kuwa, Serikali imesema kwamba, Serikali ya Ujerumani imeji- commit katika masuala matatu aliyoyasema Mheshimiwa Waziri katika jibu lake la msingi, naomba jibu kwamba, ni lini utekelezaji wa haya utafanyika, ili tuweze kujua kwa sababu, wakati anajibu amesema kwamba, majibu yalikuwa yanatolewa wakati huo kwa wakati huo. Sasa sasa hivi nataka katika hizi commitment tatu ambazo Serikali ya Ujerumani wamezitoa, ni lini sasa utekelezaji utafanyika?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hivi sasa tunapozungumza kumekuwa na tendency ya watalii kuwa wanakwenda, mwaka huu tumepokea watalii zaidi ya watano ama sita wamekwenda, lakini walikuwa wanapata kikwazo kikubwa cha barabara. Sasa Mheshimiwa Waziri haoni kwamba, kuna haja ya kujenga barabara hata kwa dharura ya kwenda kule, ili njia ikawa inapitika wakati tunasubiri hayo makubwa ambayo Serikali ya Ujerumani imeji- commit? Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Bobali kwa kuungana na Wabunge waliotangulia kabla yake, lakini pia na mawazo ya Wabunge wengine wote humu ndani ambao wana nia njema ya kuhakikisha kwamba, rasilimali na maliasili za nchi hii zinanufaisha Taifa hili. Hongera sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuhusu swali lake kwamba, ni lini hatua hizi zinazozungumziwa zitachukuliwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hatua hizi ni za majadiliano ya pande mbili. Hivi ninavyozungumza Naibu Waziri wa Mambo ya Nje alikuwa asafiri wiki hii, kutokana na changamoto nyingine za Kiserikali safari hiyo imesogezwa mbele kwa wiki moja. Atakapokwenda, matokeo ya mazungumzo hayo pengine yatakuja sasa na mpango kazi na ratiba.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vigumu kusema sasa hivi kwa upande mmoja bila kujua sasa kwa pamoja sisi sasa, Serikali ya Tanzania na Ujerumani, ratiba yetu ya utekelezaji wa haya ambayo yanaonekana kwamba tunakubaliana inaanza lini. Wakati huo utakapofika basi, utapata jawabu kwamba lini tunaanza na tunategemea kukamilisha lini programu tunayoizungumzia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika swali lake la pili, anataka mpango wa muda mfupi, kwamba, kwa sasa hivi hatuwezi kufanya utaratibu pale, hivyo hivyo palivyo kwa sababu tu za kihistoria watu wanajua kwamba alitoka mjusi mkubwa pale wa vipimo na viwango tunavyovizungumzia watu wanataka kwenda kuona kwa mazingira hayahaya yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili nafikiri nipate nafasi sasa ya kufika kwa uhalisia kabisa kwenye eneo hilo na kuona barabara hiyo inayozungumziwa, kwanza ni barabara ya aina gani. Barabara ya Mkoa, ni barabara ya Halmashauri au ni barabara ambayo jukumu lake linatakiwa kutekelezwa na nani Serikalini. Baada ya hatua hiyo tutaweza kujipanga vizuri zaidi kutekeleza, ili hayo mambo mazuri tunayokusudia yaweze kutekelezwa. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Ningependa Serikali ituambie kwa muktadha wake kabisa kwa sababu haya ambayo wameelezea kuyafanya it is a peanut! Ni madogo sana. Kujenga kituo cha Makumbusho, kuwafadhili watu kupata fani ya malikale ni hela ndogo sana! Mjusi huyu tangu apelekwe kule ni kiasi gani, kwa maana ya faida kutokana na utalii, umeiingizia Serikali ya Ujerumani? Kwa nini Serikali ya Tanzania tusiingie angalau mkataba tuwaambie angalau asilimia tano au 10 ya mapato watuletee kutokana na mjusi ambaye anaingiza fedha za utalii kule Ujerumani kuliko hizi peanut package ambazo wanatupa ambazo hazisaidii nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshauri tu Dada yangu kwamba, masuala yanayohitaji utafiti na takwimu ni vizuri kusubiri utafiti na takwimu utoe matokeo badala ya kutoa kauli za jumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa labda niseme tu kwa kifupi kwamba, mjusi huyu au mijusi hawa waliotoka Tanzania kule Ujerumani na bahati nzuri wako baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa wamefika pale mahali na mmojawapo ni Mheshimiwa Dkt. Kafumu ni kwamba, mijusi hawa wawili ni sehemu tu moja ya vivutio vingine vya malikale vilivyoko katika jumba la makumbusho kule Ujerumani ambalo ni kubwa na lina vitu vingi na kiasi ambacho hata kukokotoa kwamba, mijusi wawili wa Tanzania wanazalisha nini ndani ya jumba ambalo watu wanakuja kuangalia vitu vingi ambavyo Wajerumani hawa walivitoa katika nchi za Afrika walizotawala wakati huo katika maeneo mengi na wako wengi kwa kiasi hicho.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mambo matatu ambayo yanafahamika tayari ni kwamba, viingilio katika makumbusho ya Elimu Viumbe huko Berlin ni Euro 3.5 hadi Euro nane, kwa jumba zima ambalo lina vivutio vingi ambapo wanafunzi, watafiti na wazee wanaingia bure, hilo la kwanza.
Pili, asilimia 95 ya Bajeti ya Makumbusho ya Elimu Viumbe Berlin kule, inatoka katika Serikali Kuu na Serikali ya Mji wa Berlin, maana yake ni kwamba, hiyo makumbusho haina hata uwezo wa kuweza kujiendesha yenyewe.
Tatu, Makumbusho ya Elimu Viumbe ya Berlin ina kumbi nyingi za maonesho, Ukumbi wa Dinosauria ukiwa ni mmoja tu, kwa hiyo, ni vigumu kujua kiasi halisi cha fedha kinachopatikana kutokana na kuingia na kuona masalia ya mijusi wa Tanzania. Vilevile kwenye makumbusho hii kuna nakala ya masalia ya mijusi kutoka nchi nyingine duniani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunapozungumzia suala la kuboresha eneo hili ambako mijusi wametoka, ili liweze kuwa eneo la utalii si sahihi kusema kwamba, kipato kitakachotoka pale kitakuwa peanut. Pia, pili, ukifundisha watu kwenye taaluma hiyo ya malikale ambayo itaendelea kufanya tafiti katika nchi nzima hii, athari yake ni kubwa. Kwa hiyo, kiufupi unaweza kusema tu kwamba, watu hawa sasa badala ya kutupa samaki wanataka kutupa boti, wanataka kutufundisha kuvua, ili tuweze kuvua wenyewe samaki tupate faida zaidi kuliko kupewa samaki wa siku moja tu. (Makofi
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na kwamba kwa kweli, Naibu Waziri nadhani hili swali la Mbunge wa Tarime amelinanihii. Pamoja na dinosaur Mikoa ya Lindi na Mtwara ina utajiri mkubwa wa utamaduni ambao unaweza kutumika kama sehemu ya utalii na kufaidisha watu wa Kusini. Je, ni lini Serikali au Wizara itaamua kuanza kuwekeza kenye utamaduni wa Kusini ili utumike kama utalii wa watu wa Kusini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli Kusini ni sehemu ya maeneo yaliyoko nchi nzima, Tanzania nzima ambayo yana utajiri mkubwa wa kihistoria hasa Historia ya Utamaduni wa Mtanzania katika makabila yote tuliyonayo na kwamba, eneo hilo pia, ni kivutio cha kutosha kabisa chenye sifa ya kuweza kuwa maeneo ya shughuli za utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nirudie tu kama ambavyo nimejibu swali kama hili mara nyingi nikiwa nimesimama hapa, mbele ya Bunge lako Tukufu. Ni kwamba, Halmashauri zote, ikiwemo ile ambayo Mheshimiwa Mbunge ni Mjumbe wa Baraza la Madiwani waharakishe kutekeleza Agizo la Serikali la kuorodhesha maeneo yote ambayo yako kwenye maeneo yao, Halmashauri zao, ambayo yana sifa hizo tunazozizungumzia, ili tulete Wizarani yaweze kupitiwa, yachambuliwe, ili kuweza kuwekwa katika viwango na kuweza kuona namna gani mahitaji yake yakoje, ili tuweze kuendelea katika kuvitangaza na badaye kuwavutia watalii kwa ajili ya shughuli za utalii.