Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Ruth Hiyob Mollel (1 total)

MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, katika awamu ya nne na tano iliazishwa uboreshaji wa Serikali za Mitaa ambayo tuliita ugatuaji wa madaraka au tulikuwa tunaita D by D.

Mheshimiwa Spika, tangu wakati huo Serikali imeendelea kufanya kazi lakini ugatuaji wa madaraka haujaenda sawa sawa. Kwa mfano Serikali imechukuwa vyanzo vikubwa vya mapato vya Serikali za Mitaa; kodi ya majengo na kodi ya mabango. Je, hatua hii ambayo ilikuwa ituwezeshe Serikali za Mitaa kwa rasilimali na fedha inakinzana na dhana nzima ya ugatuaji wa madaraka?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mollel, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunazo Serikali za Mitaa zinayomajukumu yake na Serikali Kuu ambayo inawajibika pia hata kuihudumia hata Serikali ya Mitaa. Kuanzia mwaka 2014 uliousema na kufika sasa tumejifunza mambo mengi katika uendeshaji wa Serikali za Mitaa na Serikali Kuu, hasa katika utoaji wa huduma za jamii. Yapo maeneo yanahayo mafanikio, yapo maeneo yana udhaifu. Kwahiyo ni jukumu la Serikali kujiwekea taratibu wa kutibu udhahifu huu ili kuwafikia wananchi katika kuwapa huduma. Lakini bado wajibu wa kumuhudumia mwananchi kule tumewakabidhi Serikali za Mitaa ili wafanye kazi ile kwa ukaribu. (Makofi)

Sasa swali lako ni pale ambapo baadhi ya vyanzo tumepeleka Serikali Kuu kwa usimamizi bado Serikali Kuu inalo jukumu la kusimamia na hasa kwenye mapato. Serikali yetu tumeamua kudhibiti ukusanyaji wa mapato na mapato haya yarudi tena kwa wananchi, tunaporudisha kwa wananchi tunawapelekea hao hao Serikali ya Mitaa kwa mahitaji yao ili watekeleze hilo jambo, hatujawaondolea mamlaka ya kusema tunahitaji darasa, tunahitaji kituo cha afya, tunahitaji uboreshaji wa miundombinu; bado mamlaka ile tunayo.

Mheshimiwa Spika, na tumeongeza hata kuunda kwa TARURA ili isimamie miundombinu. Sasa hivi tunaenda kwenye maji isimamie utoaji wa maji. Pale ambapo kuna mahitaji Serikali za Mitaa iseme inahitaji shilingi ngapi kwa ajili ya nini, tunawapelekea. Ndiyo sababu leo tunaona huduma zinatekelezwa mpaka vijijini kwa sababu tunashirikiana na Serikali za Mitaa katika kuratibu. (Makofi)

Kwa hiyo, ule udhaifu wa usimamizi wa makusanyo, usimamizi na matumizi yake ambao ulikuwa umejitokeza sasa tunaendelea kuutibu; na ndiyo sababu unaona wakati wote tunapokwenda huko kwanza tunauliza ukusanyaji na kama makusanyo yoyote yameifadhiwa na matumizi yake, na pale ambapo matumizi yanakuwa si sahihi tunachukuwa hatua. Kwa hiyo tunakwenda tunafanya marekebisho kwa namna ya kutunza rasilimali za Watanzania zinazokusanywa kwenye maeneo haya lakini pia na matumizi yake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Mollel awe na amani kabisa kwamba tunafanya kazi kwa ushirikiano kati ya Serikali za Mitaa na Serikali Kuu kwa kuwapelekea rasilimali fedha, rasilimali watu ili ziweze kuhudumia Watanzania walioko kwenye Serikali za Mitaa huo ndio utaratibu tunaoutoa. Lakini hatujaondoa huo wajibu wa kuwahudumia wale wananchi kupitia Serikali za Mitaa. Ahsante.