Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Lucia Ursula Michael Mlowe (12 total)

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Kumekuwa na wimbi kubwa la wanafunzi wa shule za Serikali za msingi na sekondari wanaofeli kutokana na kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi katika darasa moja dhidi ya mwalimu mmoja kwa wanafunzi huku wakifundishwa kuanzia saa moja na nusu hadi saa kumi na nusu jioni, na kufanya walimu wakose muda wa kutosha wa kusimamia kazi za wanafunzi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na changamoto hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha elimu nchini kwa kupunguza msongamano wa wanafunzi madarasani, Serikali imeendelea kutenga bajeti kila mwaka kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule za msingi na sekondari. Katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali ilitenga shilingi bilioni 67.83 ambazo zimepokelewa na zimetumika ka ajili ya ukarabati, ujenzi na umaliziaji wa vyumba vya madarasa, vyoo vya walimu na wanafunzi, ujenzi wa nyumba sita (multiple unit houses) na uwekaji wa umeme (grid house solar) katika shule za sekondari 528 nchini kote. Katika bajeti ya mwaka 2016/2017 zimetengwa shilingi bilioni 48.3 kwa ajili ya kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na juhudi katika ujenzi wa miundombinu, Serikali inatarajia kuajiri walimu wapya 35,411 kwa shule za msingi na sekondari ili kuongeza idadi ya walimu hivyo kupunguza mzigo mkubwa uliopo kwa walimu kwa lengo la kuongeza tija katika sekta ya elimu hapa nchini.
MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. LUCY M. MLOWE) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Njombe - Makete kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) tayari imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina iliyofanywa na Mhandisi Mshauri, Crown Tech Consult Ltd. kwa barabara yote ya Njombe – Ndulamo hadi Makete yenye urefu wa kilometa 109.4 yakiwa ni maandalizi ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali imetenga shilingi bilioni 19 kupitia bajeti ya maendeleo kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa Barabara ya Njombe - Ndulamo - Makete, na ninaomba kulishukuru Bunge lako, kiwango hiki mmekipitisha.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Jeshi la Zimamoto Mkoani Njombe linakabiliwa na ukosefu wa Ofisi pamoja na vitendea kazi hususan magari jambo linalopelekea Jeshi hilo kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi.
Je, ni lini Serikali italipatia Jeshi hilo ofisi za kudumu pamoja na magari ili liweze kutoa huduma nzuri kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji lina uhaba mkubwa wa ofisi na vitendea kazi katika vituo vyote nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni nia ya Serikali kuongeza bajeti kwa Jeshi la Zimamoto na uokoaji ili liweze kukabiliana na changamoto zilizopo zikiwemo uhaba wa vitendea kazi kama vile magari ya kuzimia moto, magari ya maokozi pamoja na kufanyia ukarabati ofisi zilizopo katika mikoa yote na kuliwezesha Jeshi la Zimamoto kuwa la kisasa ili kutoa huduma nzuri kwa wananchi wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nia hii njema ya Serikali itakuwa ikitekelezwa kwa mujibu wa upatikanaji mapato ya Serikali na bajeti itakayotengwa kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kila mwaka.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Kilimo cha viazi katika Mkoa wa Njombe kimekuwa ni ukombozi kwa wananchi wa mkoa huo. Zao hilo ni la biashara lakini wananchi wameanza kukata tamaa kutokana na kupanda kwa bei za pembejeo, pembejeo kutokufika kwa wakati na kukosa soko la uhakika:-
Je, Serikali ipo tayari kuwaunganisha wakulima hao na kuwa na chama chao kitakachoweza kupigania haki za wakulima hao?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikihimiza makampuni na mawakala wanaosambaza pembejeo za kilimo kuwafikishia pembejeo wakulima kwa wakati kabla ya msimu wa kilimo kuanza. Kutokana na juhudi ya Serikali kwa kushirikiana na makampuni yanayosambaza pembejeo, imewezesha ufikishwaji wa pembejeo ikiwemo mbolea na mbegu bora kwa bei ya soko kwa wakulima kwa wakati. Aidha, changamoto ya kupanda bei ya pembejeo inafanyiwa kazi kwa kuondoa tozo mbalimbali ili kupunguza bei ya pembejeo na kuwezesha wakulima kumudu kununua na kutumia pembejeo hizo. Vilevile Serikali inakamilisha mchakato wa manunuzi ya pamoja (bulk procurement), uondoaji au kupunguza tozo mbalimbali na gharama za usafirishwaji katika mbolea ambao utasaidia kuongeza upatikanaji na kupunguza bei ya mbolea.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea kuhimiza uzalishaji wa mbegu za viazi kupitia vikundi katika ngazi ya mkulima. Kupitia utaratibu huu wakulima wengi watamudu kununua mbegu za viazi kwa bei nafuu kwa vile zinazalishwa ndani ya kijiji. Pia kupitia SAGCOT wakulima nane wamepata mafunzo ya kuzalisha mbegu za viazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ambazo zitauzwa ndani ya mkoa na hivyo kuchangia upatikanaji wa mbegu za viazi kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari kuwaunganisha wakulima wa zao la viazi kwa kutumia taasisi zake katika kuunda ushirika ambao utasaidia kuanzisha chama chao kulingana na taratibu za uanzishwaji wa vyama vya ushirika. Jukumu hili litatekelezwa kupitia tume ya ushirika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Halmashauri husika katika Mkoa wa Njombe.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Mgogoro wa Kiwanda cha Chai Lupembe umewaathiri wakulima wa chai Lupembe na Wilaya nzima ya Njombe kutokana na kukosa soko la zao la chai.
Je, Serikali ipo tayari kujenga kiwanda kingine cha chai kunusuru uchumi wa wakulima wa chai katika Wilaya ya Njombe?
WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuwa migogoro inaathiri sana shughuli za uzalishaji viwandani pamoja na kuwaathiri wakulima ambao hukosa soko la malighafi zinazozalishwa. Kiwanda cha Chai Lupembe ambacho kilikumbwa na mgogoro wa muda mrefu uzalishaji ulisimama kwa miaka nane kati ya 2008 na 2015. Katika kipindi hicho na baada ya Serikali kuona wakulima wanakosa soko la majani ya chai, Serikali ilishawishi Kampuni ya Mufindi Tea and Coffee Ltd. kujenga kiwanda cha chai, katika tarafa ya Lupembe, Kijiji cha Ikanga.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hicho kilijengwa na kuanza usindikaji wa majani ya chai mwaka 2013. Hata hivyo, kufuatia hukumu ya Mahakama iliyompa ushindi mwekezaji wa kampuni ya Dhow Merchantile East Africa Ltd., na Lupembe Tea Estate Ltd. dhidi ya Muungano wa Vyama vya Ushirika vya Lupembe, mwezi Januari, 2016 uzalishaji katika kiwanda hicho ulianza na unaendelea. Kwa sasa kuna kesi mahakamani inayoendelea kusikilizwa kufuata rufaa ya MUVYULU dhidi ya ushindi aliopata mwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na viwanda vya kutosha ili kuchochea kilimo cha zao la chai na usindikaji wa majini ya chai katika Mkoa wa Njombe anakotoka Mheshimiwa Lucia Mlowe ambao una utajiri mkubwa wa zao hilo. Hivyo, Serikali imendelea kuhamasisha uwekezaji katika mkoa huo. Kampuni ya Unilever imeanza ujenzi wa kiwanda kipya cha chai. Kiwanda hicho kinatarajia kuanza uzalishaji mwaka 2018 na kitatoa ajira zipatazo 300.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwekezaji anatarajia kuanzisha mashamba ya chai yenye ukubwa wa Ekari, 1,000. Kati ya hizo ekari 200 zimeshapandwa mbegu za chai. Hivyo wakulima wa zao la chai wa Wilaya ya Njombe watapata fursa ya kuuza mazao katika kiwanda hicho kipya cha Unilever kitakapokamilisha ujenzi sambamba na viwanda vya Lupembe Tea Estate Ltd. na Ikanga chini ya Kampuni ya Mufindi Tea and Coffee Ltd.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulieleza Bunge lako Tukufu na Waheshimiwa Wabunge wanaotoka maeneo yanapolimwa majani ya chai kuwa Serikali inafuatilia kwa makini chanzo cha migogoro katika mashamba hayo na kuitatua na kuipatia suluhu ya kudumu.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Msongamano wa magari, ujenzi holela, miundombinu duni ya maji taka na kadhalika katika miji mikubwa hapa nchini vinatokana na udhaifu wa upangaji wa matumizi bora ya ardhi (poor land use planning).
Je, Serikali imejiandaa vipi kuendesha zoezi la Mipango Miji na matumizi bora ya ardhi katika miji mipya ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Njombe?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kifungu Namba 7(1) cha Sheria ya Mipango Miji Na. 8 ya mwaka 2007 kinaelekeza kuwa jukumu la upangaji na uendelezaji miji lipo chini ya mamlaka za upangaji ambazo ni Halmashauri za Majiji, Manispaa Miji, Wilaya na Mamlaka za Miji Midogo. Kutokana na umuhimu wa kuwa na Miji iliyopangwa kiuchumi na kijamii, Serikali imechukua hatua mbalimbali ikiwemo uandaaji wa mipango kabambe itakayotumika kuongoza, kusimamia na kudhibiti uendelezaji wa Miji pamoja na urasimishaji wa makazi yasiyopangwa katika maeneo mbalimbali nchini.
Hadi kufikia Oktoba 20, 2017 maandalizi ya mipango kapambe ya miji 29 nchini ilikuwa imefikia katika hatua mbalimbali. Maeneo hayo ambayo tayari mipango yake ipo katika hatua mbalimbali ni Majiji ya Mwanza, Da es Salaam, Arusha na Tanga na kwa upande wa Manispaa tunayo Mtwara - Mikindani, Iringa, Musoma, Tabora, Singida, Sumbawanga, Songea, Shinyanga, Morogoro, Lindi, Bukoba, Moshi, Mpanda na Kigoma Ujiji. Kwa upande wa miji midogo ni Kibaha, Korogwe, Njombe, Bariadi, Geita, Babati, Ifakara, Mahenge, Malinyi, Tunduma na Mafinga. Kati ya maeneo hayo, mipango kabambe kwa Manispaa ya Mtwara - Mikindani, Musoma, Iringa na Singida imeshaidhinishwa na kuzinduliwa na hivyo imeanza kutumika rasmi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uandaaji wa mipango kabambe hufanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali yakiwemo makampuni ya upangaji na upimaji ardhi yaliyosajiliwa kwa mujibu wa sheria, wamiliki wa ardhi, taasisi za Serikali, watu binafsi na asasi za kiraia pamoja na taasisi, zinatoa huduma mbalimbali za miundombinu kama vile TANESCO, TANROADS na Mamlaka za Maji Safi na Maji Taka. Utekelezaji wa mipango hiyo husaidia kutatua changamoto zilizopo na hatimae kuwa na miji iliyopangwa na yenye mtandao mzuri wa miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango kabambe wa Mji wa Njombe unaandaliwa na Kampuni ya CRM Land Consult ya Dar es Salaam kupitia programu ya Urban Local Government Strengthening Program iliyofadhiliwa na Benki ya Dunia chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Hadi sasa rasimu ya kwanza ya mpango kabambe ya mji huo imeandaliwa na hatua inayofuata ni kuwasilisha rasimu hiyo kwenye mikutano ya wadau kwa ajili ya kupokea maoni na mapendekezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa wito kwa mamlaka za upangaji ambazo hazina mipango kabambe, kuanza maandalizi ya mipango hiyo pamoja na kongeza kasi ya kupanga maeneo mapya, kurasimisha makazi yasiyopangwa na kudhibiti uendelezaji holela kwa kushirikiana na makampuni yaliyosajiliwa kufanya kazi hiyo kwa mujibu wa sheria.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Ardhi ya Njombe inahitaji mbolea kwa wingi zaidi kuliko mikoa mingine.
Je, Serikali ina mkakati gani wa uanzishaji wa Kiwanda cha Mbolea Mkoani Njombe?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbolea ya viwandani inatokana na malighafi za madini. Aina za mbolea hizo ni nitrogen inayotengenezwa kwa kutumia ammonium inayokana na gesi asilia, mbolea ya phosphorous na ile ya phosphate. Tanzania ina kiwanda kimoja kikubwa cha mbolea cha Minjingu Mkoani Manyara kinachotengeneza mbolea aina ya phosphate kutokana na malighafi husika kupatikana mkoani humo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na upatikanaji wa soko la mbolea Mkoani Njombe, tafiti za kijiolojia zinaonesha kuwa malighafi za phosphate, phosphorous na gesi asilia hazipatikani mkoani humo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kujenga viwanda vingine vya mbolea, majadiliano na wawekezaji wa kampuni za HELM na FERROSTAAL ya Ujerumani zinaendelea kwa ajili ya ujenzi wa viwanda viwili katika Mikoa ya Mtwara na Lindi kutokana na upatikanaji wa gesi asilia. Hivyo ni vyema Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na mkoa na halmashauri kuhamasisha uwekezaji unaolenga zaidi kujenga viwanda vya kuongeza thamani ya malighafi zinazopatikana kwa wingi katika mkoa huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo mkoa mmoja utakuwa soko la bidhaa za mkoa mwingine kama itakavyokuwa kwa mbolea kutoka Lindi na Mtwara wakati Mkoa wa Njombe ukitoa mazao ya chakula, matunda na mazao ya mbao. Serikali inaendelea kuvutia wawekezaji katika viwanda vya mbolea ili kutosheleza mahitaji ya nchi nzima.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Mfumo wa mabomba ya maji kwenye maeneo mengi nchini ni chakavu hivyo kusababisha upotevu mkubwa wa maji:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha mabomba yote chakavu katika nchi ili kuokoa maji yanayopotea kutokana na uchakavu huo?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli sekta ya maji imekuwa inakabiliwa na changamoto ya upotevu wa maji kutokana na uchakavu wa miundombinu iliyojengwa miaka mingi iliyopita. Katika kukabiliana na changamoto hizo, Serikali imeendelea na jitihada za uwekezaji katika ukarabati wa miundombinu chakavu maeneo mbalimbali ya mijini ikiwemo Mikoa ya Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Mwanza, Morogoro, Singida pamoja na ukarabati wa miradi ya kitaifa ya Makonde, Wanging’ombe, Maswa, HTM, Mugango Kiabakari na Chalinze.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Miradi ya Maji Vijijini, Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo imeendelea kuimarisha Programu ya Uendelevu wa Huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini kwa kutumia Mfumo wa Malipo ya kwa Matokeo (Payment for Results -PforR na Payment by Results – PbR) ambapo kwa pamoja zinalenga kuhakikisha kasi ya uendeshaji, matengenezo na ukarabati wa miundombinu ya miradi ya maji vijijini inakuwa endelevu na wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada hizo kwa pamoja zitasaidia kupunguza hali ya upotevu wa maji katika miradi ya maji mijini na vijijini.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-
Wapo Watumishi katika sekta ya afya, hususan Madaktari na Wauguzi ambao waliajiriwa katika miaka ya 1980 kupitia Serikali Kuu, lakini wakati ule hapakuwa na makato ya mfuko wa kijamii na kuanzia mwaka 1999, Serikali ilianza kuwakata mishahara yao kwenye Mfuko wa PSPF:-
Je, Serikali inawafikiriaje Watumishi hao ambao fedha zao hazikukatwa na mifuko ya kijamii wakati huo hususan Mfuko wa PSPF?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya Julai 1999, mfumo wa malipo ya mafao ya kustaafu kwa watumishi wa Serikali Kuu haukuwa wa kuchangia. Kwa mantiki hiyo, watumishi wote wa umma waliokuwa kwenye ajira ya masharti ya kudumu wanastahili malipo ya uzeeni, wakiwemo watumishi wa sekta ya afya hata kama hawakuchangia. Aidha, kwa mujibu wa Ibara ya tano (5) ya Sheria ya Mfuko wa Pensheni wa PSPF, watumishi wote wa Serikali Kuu ambao waliajiriwa na kuthibitishwa katika ajira ya masharti ya kudumu na pensheni, wanakuwa wanachama wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF kuanzia tarehe ya kuanzishwa kwa mfuko huo.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mafao ya Hitimisho la Kazi Na.2 ya Mwaka 1999 kwa Watumishi wa Umma, ambayo ilianzisha Mfuko wa Pensheni wa PSPF, wastaafu wote ambao ni wanachama wa Mfuko wa Pensheni wa PSPF na wanaoguswa na Sheria hii wanalipwa mafao yao ya kustaafu na Mfuko wa Pensheni wa PSPF kwa kipindi chote cha utumishi wao. Hii inamaanisha kwamba, mafao yao yanakokotolewa kuanzia tarehe ya kuajiriwa hadi wanapostaafu utumishi wao kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Utumishi wa Umma.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-

Uwanja wa Ndege wa Njombe umekuwa kero kwa wananchi, kwani upo katikati ya Mji na haujakarabatiwa kwa muda mrefu matokeo yake uwanja huo umejaa barabara hizo. Aidha, watu wanaopita katika barabara hizo zisizo rasmi hukamatwa na kutozwa faini:-

Je, ni lini mkakati wa Serikali juu ya uwanja huo ili kupunguza kero kwa wananchi hao?
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanja cha ndege cha Njombe kilijengwa na Wakoloni, yaani kabla ya uhuru miaka ya 1940 na kuanza kutumika rasmi 1945. Miaka hiyo Mji wa Njombe ulikuwa mdogo sana na hivyo kiwanja kilikuwa mbali na makazi ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria za Kitamaifa za Usalama wa Anga hairuhusiwi watu, wanyama, magari na kadhalika kukatiza kwenye viwanja vyovyote vya ndege. Kwa mantiki hiyo, vitendo vya baadhi ya wananchi wa maeneo hayo kukatiza katika kiwanja hicho ni vya uvunjivu wa sheria na ndiyo maana wananchi hao hukamatwa na kutozwa faini au kuadhibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika juhudi za kukarabati kiwanja cha ndege cha Njombe, Serikali imepanga kufanya upembuzi yanikifu na usanifu wa kina kwa kutumia fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia uliohusisha pia viwanja vya ndege vya Iringa, Songea, Lindi, Kilwa Masoko, Tanga, Moshi, Lake Manyara, Singida, Musoma na kiwanja kipya cha Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina imekamilika kwa viwanja hivyo ambapo taarifa ya mwisho iliwasilishwa tarehe 28 Machi, 2017. Hatua iliyopo kwa sasa ni utafutaji wa fedha kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa kiwanja hicho. Upanuzi huo utahusisha ujenzi wa uzio kuzunguka eneo lote la kiwanja ili kudhibiti wananchi wanaokatisha kiwanja hicho kinyume cha taratibu.
MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:-

Barabara za Makete Njombe na Itone - Ludewa zipo katika ujenzi lakini ujenzi huo unakwenda pole pole sana:-

Je, ni lini ujenzi wa barabara hizo utakamilika?
NAIBU WAZIRI, UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Njombe - Makete kilometa 107.4 umejengwa katika sehemu mbili za Njombe - Moronga kilometa 53.9 na Moronga - Makete kilometa 53.5 ili kuharakisha utekelezaji wake. Hatua ya utekelezaji inayofikiwa hadi Machi, 2019 ni asilimia 25.2 ambapo kazi zinatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Januari, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi kwa kiwango cha zege wa barabara ya Itoni – Ludewa – Manda sehemu ya Rusitu - Mawengi kilometa 50 umefikia asilimia 20.14. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2020. Napenda nimkahakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Wizara kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) itaendelea kuwasimamia Wakandarasi wa miradi hii ili waweze kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo kwa wakati uliopangwa.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST (K.n.y. MHE. LUCIA M. MLOWE) aliuliza:-

Njombe ni kati ya Mikoa mikubwa ya Kilimo na ina mashamba darasa ambapo wanafunzi wa maeneo mengine wanakuja kujifunza:-

Je, ni lini Serikali itaanzisha Chuo cha Kilimo katika Mkoa wa Njombe?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua mchango wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Mkoa wa Njombe katika uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara. Kutokana na umuhimu huo Serikali ilianzisha vyuo vitatu vya Kilimo katika Nyanda za Juu Kusini ambayo Mkoa wa Njombe umo, ili kuzalisha wataalamu wa Ugani watakaotoa huduma za ushauri kwa wakulima katika mikoa hiyo. Vyuo hivyo ni MATI Uyole, Igurusi na Inyala vyenye uwezo wa kudahili wanafunzi takribani 700 kwa wakati mmoja. Hata hivyo, vyuo hivyo vinadahili wanafunzi chini ya uwezo kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo uchakavu wa miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilianzisha Chuo cha Wakulima cha Ichenga mkoani Njombe kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa wakulima. Kwa sasa Serikali haina nia ya kuanzisha chuo kipya cha kilimo katika Mkoa wa Njombe wala kwenye kanda yoyote ile, badala yake Serikali ina mpango wa kuviboresha vyuo vya kilimo vilivyopo, kikiwemo Chuo cha Wakulima cha Ichenga kwa kuvikarabati na kuviwezesha kifedha, ili viweze kuchukua wanafunzi na wakulima kwa ajili ya mafunzo ya rejea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali itaendelea kushughulikia changamoto katika vyuo vya kilimo ili kufikia lengo la kuwa na wataalamu wa kilimo wa kutosha na hivyo kufanikisha mapinduzi ya kilimo hapa nchini. Vile vile, Serikali inafanya ukarabati kwa chuo cha MATI Inyala kwenye Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ambapo Mkoa wa Njombe upo.