Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Riziki Saidi Lulida (49 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RIZIKI S.LULIDA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nakushukuru na namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia kupata afya njema.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nashukuru kwa hoja iliyowekwa mezani, ni nzuri, lakini namwonea huruma sana shangazi yangu Mheshimiwa Mwijage kuwa atapambana na kazi kubwa sana katika suala la viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na-declare Interest, mimi ni Mjumbe katika Kamati ya Uwekezaji. Nimeangalia Uwekezaji na Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma na Taasisi zake kama ni mwiba unaoitafuna nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeingia katika uwekezaji tukikurupuka, mikataba mibovu, usimamizi mbovu, corruption ndiyo imesimama. Leo tuna Taasisi zaidi ya 200 katika uwekezaji, lakini mpaka sasa hivi ni mashirika machache sana ambayo yanaweza yakatoa faida katika nchi hii. Taasisi hizo naweza nikazitaja ambazo angalau zimeonesha zinaweza zikatupeleka mbele katika dira ya maendeleo ya uwekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, moja, ni TANAPA. Inapeleka ruzuku katika pato la Taifa; Ngorogoro inatoa Ruzuku katika pato la Taifa; National Housing Corporation inatoa ruzuku katika pato la Taifa na NSSF. Sasa tujiulize, Taasisi nyingine zinategemea ruzuku kutoka Serikalini, kulikuwa na haja gani ya kubinafsisha wakati bado wanakula fedha ya Serikali na zinaingia katika mashirika yao? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuangalia Taasisi nyingi tulizokuwa nazo, hazina Bodi. Bodi ni dira, sasa kama Shirika halina Bodi unategemea nani ataendesha usukani wa Shirika lile? Nani atasimamia matumizi katika shirika lile? Kwa nini tumekaa na mashirika kwa muda mrefu yakiwa hayana Bodi? Nataka nipate majibu katika Taasisi zote kwa nini hazina Bodi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeangalia Taasisi nyingi hazina Business Plan, uliingiaje katika mkataba wa ubinafisishaji na uwekezaji hakuna Business Plan? Matokeo yake unakuta mashirika ambayo hayahusiki na ujenzi wa majumba, sasa hivi wanakimbilia kujenga majengo. Sasa National Housing ipo, NSSF ipo, kwa nini unajenga nyumba sasa hivi? Ni kutokuwa na mwelekeo wa Business Plan yake; sivyo inavyokwenda! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaingia katika suala la Mashirika mbalimbali ambayo tumeangalia. Katika kuyaangalia kwa kweli unapata huruma! Mashirika mengi yana uwezo mdogo wa Watendaji, inaonekana hawana capacity ya kuliongoza Shirika. Kwa nini umempa taasisi mtu ambaye hana uwezo? Matokeo yake, yale mashirika haya-perform. Kama hamjafanya kazi ya kuangalia nani ana-perform, nani ha-perform ina maana tutaendelea kuwa na business as usual. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nilizungumzie Shirika la TANESCO. Shirika la TANESCO wameingia wawekezaji wakubwa, mmojawapo IPTL, Songas, Symbion, wako pale kulila lile shirika. Tufikie mahali tujiulize, nani aliweka ule mkataba mbovu mpaka kufikia hili shirika lisiweze ku-perfom? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, itakuwa kila mwaka; mkataba wa Songas unasikitisha, anasema, mimi nimechukua mkopo, hivyo sitarudisha mkopo ule niliochukuwa Tanzania mpaka kwanza TANESCO anilipe. Bei anayotoa na ya kununulia ni vitu viwili tofauti. Anatoa Dola 13, huyu analipa Dola 21; jamani ni mkataba gani huu? Mnampa mkataba huu mpaka 2020/2025 toka alipoanzia, hana ruhusa ya kuguswa. Jamani, Watanzania tunajipenda hatujipendi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna huruma na nchi yetu au hatuna huruma na nchi yetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja katika Bodi ya Sukari. Bodi ya Sukari imekaa pale tu kama bodi lakini haina meno, kazi inafanywa na Wizara. Wizara ndiyo wanatoa vibali vibovu vyote vya sukari. Sukari inaandikwa inakwenda nje ya nchi, kumbe inauzwa Tanzania hapa hapa, sukari inaletwa kama malighafi, siyo malighafi, iko katika viwanda. Wanachofanya, inatembea karatasi, sukari ikishateremshwa karatasi inapita katika vituo vyote kama Lorry hii imepita na sukari mpaka inafika Tunduma, lakini sukari iko bado mjini hapa! Kwa faida ya nani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tujiulize na sisi Watendaji ambao Watanzania wote wamekosa uzalendo, ndiyo maana wenzetu Kenya wanatupita au Rwanda wanatupita; uzalendo wa Watendaji ni mdogo sana! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja katika upande wa viwanda. Mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani tulikuwa na Viwanda vya Korosho 13, vile viwanda vyote vimefungwa. Matokeo yake, kama Mkoa wa Lindi, hatuna ajira kwa viwanda hivyo. Hata kiwanda kimoja Lindi hamna! Unategemea wale Wamachinga watakwenda wapi? Wakija Dar es Salaam wanafukuzwa! Lindi viwanda mmevifunga, wanakwenda wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, ile korosho sasa, ule ndiyo mwiba, amepewa sura pana ananunua korosho vijijini sasa hivi! Wanapewa kununua ufuta vijijini! Hivi jamani panya umemwingiza kwenye ghala, unategemea nini? Ufuta sasa hivi hauna bei maalum, ufuta umelimwa vya kutosha, lakini sasa hivi unaambiwa sh. 1,300/= ukienda hapa sh. 2,000/=. Matokeo yake hata soko la ufuta hakuna! Tunategemea kuletewa mafuta mabovu kutoka nje! Hivi jamani mnaziona cancer zilizojaa Tanzania? Magonjwa ya figo mnayaona yalivyojaa Tanzania? Tunakula mafuta machafu, ufuta wetu tunaupeleka nje ya nchi. Tujiulize, tuna vision? Tuna mission? Are we responsible? We are not responsible. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumefikia mahali tuko business as usual. Naomba tuambiwe, ule ufuta ambao umezalishwa, maana yake sasa hivi Tanzania ni nchi ya pili kuuza ufuta duniani, lakini tunaagiza mafuta kutoka nje; kwa sababu gani tunakula mafuta mabovu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini mnatuendeleza mpaka leo tunakula mafuta machafu wakati tuna ufuta, karanga, pamba na alizeti; ni kwa sababu gani mnatufanyia mambo kama haya? Mko serious? Hamko serious, mmekaa kuangalia corruption, nitapata bei kiasi gani, nitapata fedha kiasi gani, basi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, masikitiko yangu makubwa, naangalia vijana ambao wanayumba yumba. Hizi korosho zinapelekwa nje kama raw material, tunapeleka ajira nje! Wanafanya makusudi kuhakikisha Mtanzania hapati ajira katika nchi hii. Wakiwa na viwanda vyao, Mtanzania hana nafasi! Ufuta wetu ambao ni bora, korosho zetu zilizokuwa bora, pamba tunapeleka nje ili kutoa ajira nje. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka majibu, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kumalizia aniambie, ajira ya vijana kwa viwanda mlivyofunga itapatikana lini? Tujiwekee time frame kwa vile viwanda vilivyofungwa vya Mtwara, Masasi, Nachingwea, Lindi na Kibaha vitafunguliwa lini ili tuone kweli makucha yapo? Kama havijafunguliwa, mwakani nitauliza tena swali hili hili! Vijana wanazurura, wanahangaika!
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikwenda Nachingwea, tulikuwa katika msafara wa viongozi, maghala yale ndani mna mbao mpaka juu. Jiulize, yeye amepewa kiwanda kwa ajili ya korosho, zile mbao zinafanya kazi gani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Viwanda vya Urafiki; tumekwenda Urafiki vile viwanda ndani kumejaa ma-pampers na vitu vingine. Je, tuna vision na biashara zetu? Business Plan zetu zinasema nini? Yule wa Kiwanda cha Urafiki alikuwa atengeneze nguo, amejaza na viwanda; amechukuliwa hatua gani? Tunataka tujue, hatua gani amechukuliwa? Kama hatujajua amechukuliwa hatua gani, itakuwa ni watu ambao wanaachwa. Anakamatwa na pembe, mnaambiwa, bwana, hajui Kiswahili, ndiyo maana yake tunavyofanya sasa hivi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vyetu havina thamani, vimekuwa maghala, watu wanaweka vitu vingine; hivyo kilichowekwa pale siyo. Tunataka tujue Action Plan, Business Plan zetu zinakwendaje? Tupo kwa kujenga au tupo kuwaachia wageni na uwekezaji wao uwe wa kutubomoa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nawashukuruni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye amenijalia na mimi kuchangia katika hoja iliyopo mezani. Katika falsafa ya uchumi wanazungumza hivi, we need to plan for future and not for wait and see attitude. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi, Mkoa wa Mtwara, Mkoa wa Ruvuma ndiyo mikoa ambayo iliachwa nyuma katika maendeleo, hasa katika suala la miundombinu, lakini Mwenyezi Mungu hii mikoa ameipa neema kubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na Mkoa wa Lindi. Tumeingia katika uwekezaji mkubwa wa viwanda vya LNG na kutoa nafasi kubwa kwa wawekezaji kwenda kuwekeza katika Mkoa wa Lindi. Cha kusikitisha, kwa nini ninasema we don’t plan for future we are planning for wait and see attitude, kiwanja cha ndege kiko karibu na uwekezaji wa viwanda, hakimo ndani ya kitabu hiki. Sasa unajiuliza, mwekezaji anahitaji kutoka Dar es Salaam kwenda Kikwetu, uwanja ambao ni mkubwa, wa pili katika Afrika, ule uwanja ulikuwa unatumika, ndege zikitoka Ulaya zinateremka Kikwetu, zikitoka Kikwetu zinakwenda South Africa, angalieni ndani ya Encyclopedia Britannica inakupa taarifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ule uwanja umetupwa kwa miaka yote 50, halafu mnakwenda kuwekeza maeneo hayo. Hapa mmetufunika tu, tutakwenda kurekebisha uwanja wa ndege wa Kikwetu, sijui wa Lindi, wa Kilwa, tumejipanga? Hatujajipanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kuingia katika uwekezaji mkubwa wa gesi na tumeambiwa Tanzania tumepata trilioni tano gesi, lakini hatuna uwekezaji katika eneo lile, hata uwanja wa ndege haupo. Wanataka kutumia viwanda Bandari ya Lindi haipo, Bandari ya Kilwa haipo, Airport ya Kilwa haipo, tunawekeza nini hapo? Hizi ni bla bla.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunakuja suala la mawasiliano. Huamini ukifika Airport ya Kikwetu hakuna mawasiliano. Wanapoweka Kiwanda cha Likong‟o hakuna mawasiliano, huyo mwekezaji anakuja kufanya kazi gani pale? Bila kuwa na mtandao anafanya kazi gani? Wanakwenda kisasa, wanakwenda kidijitali sisi tunakwenda kianalogia, tumefika katika uwekezaji? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, reli. Katika maisha yangu sijapata kusikia tatizo lililofanyika reli kutoka Mtwara ikang‟olewa, waling‟oa kwa sababu gani? Kwa nini wasingeiacha? Leo tunataka kuwekeza katika mazao ambayo yatatoka Nachingwea, Liwale, Ruangwa yanapelekwa Bandari ya Mtwara, reli hamna. Wananchi wanaingia katika kutumia gharama kubwa ya kukodi magari kupeleka ufuta wao ukanunuliwe Mtwara wakati reli ilikuwepo Nachingwea. Hapa sijaiona reli ya Nachingwea inarudishwaje pale ili kuwarahisishia wananchi waweze kuingia katika hali bora ya maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia suala la barabara katika mikoa ya kusini. Katika ilani na ahadi zilizotolewa na Rais kuwa barabara ya kutoka Nangurukuru kwenda Liwale mpaka Nachingwea itapatikana lami. Leo mtu anakwenda Liwale, sasa hivi mvua zimekwisha ndiyo mtu wa Liwale anaweza kwenda Liwale; lakini inambidi atoke Dar es Salaam mpaka Lindi, Lindi mpaka Masasi, Masasi – Nachingwea ndipo anakwenda Liwale. Jamani hata huruma hatuwaonei hawa watu? Wakisema hawako Tanzania wako Tanganyika mtakubaliana nao watu wa Liwale wako Tanganyika. Hawawezi kwenda Liwale, nauli ya kwenda Liwale utafikiri anatoka hapa anakwenda Kampala wakati anakwenda sehemu ya karibu tu hapa. Na ahadi zimetolewa za uwongo kwa muda mrefu. Tufike mahali tuachane na uwongo twende na ukweli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Waziri mwenye mamlaka aniambie ni lini barabara ya Liwale itajengwa kwa lami? Tumechoka na ahadi za uongo ambazo hazikamiliki. Kama ni maisha bora ya Watanzania hata mtu wa Liwale anahitaji maisha bora, hata wananchi wa Nachingwea wanataka maisha bora, hata mwananchi wa Ruangwa anataka maisha bora. Tunataka barabara za lami zifike katika maeneo, Mkoa wa Lindi wote hauna barabara za lami, haiwekezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaingia katika suala la mazao, anatoaje mazao kutoka vijijini kwenda barabara kubwa, hakuna barabara. Nimejaribu kuleta maswali wakasema watatoa pesa hakuna pesa iliyofika mpaka sasa hivi. Nangalu – Chikonji waliniambia tutatoa milioni 700 hakuna pesa. Mchinga – Kijiweni hakuna pesa iliyopelekwa, Mkwajuni Mipingo hakuna pesa iliyopelekwa kule, tunaingiaje katika uwekezaji hakuna hata mazingira bora ya barabara na mawasiliano hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunataka kuwekeza kilwa na ndilo eneo la pili limeonekana bora katika uwekezaji, hakuna usafiri bora unaozunguka katika maeneo ya Kilwa. Kwenda Njinjo, kwenda Kandawale, kwenda Mitole, utafikiri eneo lile halijapata uhuru katika miaka 50. Watu wako katika mazingira magumu, kuna ubaguzi mkubwa unafanyika katika kugawa miradi. Kuna mikoa inapata upendeleo, Mkoa wa Lindi kila siku wa mwisho, lakini Mungu ameleta ruzuku ya neema, hii neema mnaifanya nini? Neema hii haitamsaidia mtu wa Lindi, itatusaidia Tanzania nzima, tufike mahali tutathmini tulijipanga kwa future au tumejipanga for wait and see attitude? Haikubaliki.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Waziri mwenye dhamana aniambie katika uwekezaji alioupeleka Lindi anataka kutupatia kitu gani Lindi, amejipanga vipi kuhusu mawasiliano, kuhusu uchukuzi, amejipanga vipi kuhusu barabara, nitawaelewa kama kweli mnataka maendeleo, lakini bila hivyo sijaona kama kuna juhudi za kikamilifu za kupeleka maendeleo Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Lindi ni Mkoa ambao sasa hivi unaona neema, lakini unaona mipango iliyopangwa ya hovyo hovyo, tunahitaji mabadiliko ya kweli na ya dhamira ya kumkomboa mwananchi wa Lindi na Tanzania kwa Ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunakuja suala la maendeleo ya barabara, nilileta maswali hapa wakasema fedha tayari zimeshapelekwa Lindi naomba Waziri mwenye dhamana aniambie ni fedha gani zimepelekwa Lindi vijijini kwa ajili ya zile barabara? Sasa hivi Ufuta huko vijijini unashindwa kuja mjini, barabara hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Nangaru leo wamekaa na ufuta vijijini wanatafuta barabara, hawana! Sasa tutafutieni njia maana yake tumejaribu kuongea imekuwa kama tumemfungia kengele mbuzi , tunaomba majibu yenye dhati, ni lini daraja la Mchinga, kijiji cha muda mrefu, Makao Makuu ya Jimbo hakuna daraja la kutoka Mchinga kwenda Kibiweni, Mheshimiwa Rais mwenyewe Magufuli alifika Lindi akasema nitajenga hili daraja la Mchinga na mimi ni mlezi wa hapa, naomba Waziri mwenye dhamana alimalize daraja la Mchinga na watu wa Mchinga waneemeke. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ahsanteni sana.
Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia hii nafasi. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kunipatia afya njema. Ukimuona mtu mzima analia basi ujue amepatwa huyo mtu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka ni-declare interest kama mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PIC au Uwekezaji. Kwa kweli, kama ingekuwa Wabunge wote wanapata taarifa za mikataba mibovu ambayo imeingiwa na mashirika mbalimbali basi, humu ndani tusingekuwa pamoja tungekuwa tumepata msiba mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitu ambacho nimejifunza katika kukaa katika Kamati ya Uwekezaji, kwanza ni mikataba mibovu ambayo imeifanya nchi isiweze kwenda. La pili, tumeshindwa kusimamia Sheria ya Uwekezaji. Tatu, kulindana kulikopitiliza, matokeo yake wanapewa watu nafasi ambao hawawezi kuzifanyia kazi, iwe Mwenyekiti wa Bodi au awe Mkurugenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na ninakotoka, Mkoa wa Lindi na Mtwara. Mkoa wa Lindi na Mtwara tulikuwa na viwanda vya korosho vinane na wawekezaji au ubinafsishaji wakapewa vile viwanda kwa bei ya kutupa. Tangu walipopewa viwanda vile wamevifungia mpaka leo, je, Serikali ipo, haipo? Serikali ina macho, haina macho? Lakini wamelifumbia macho na kuacha viwanda vile vikifungwa mpaka leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamewapa wawekezaji, wale wawekezaji wamevifunga vile viwanda, wametoa mashine na kuzipeleka Mozambique ambako wamefungua viwanda vingine na kuwaacha watu wa Mtwara na Lindi wakiwa hawana ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza watu wale wale wamepewa kazi ya kupeleka korosho nje as a raw material, tujiulize tunajitambua? Kama kweli tunakwenda katika uwekezaji wa viwanda kwa mfumo huu hatutoki, maana mnawajua nani anasafirisha korosho nje, anapeleka ajira nje, anapeleka kila kitu nje, viwanda amevifungia kwa sababu ya nani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Waziri mwenye dhamana atuambie kwa nini viwanda hivi vimefungwa zaidi ya miaka kumi wananchi hawana ajira na korosho inapelekwa nje ajira inapelekwa nje?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii haikubaliki ni aibu. Lazima tujitambue na tufunguke, kwa hiki tunachofanyiwa ni aibu. Hata kama utasema tunataka kuwekeza kama mikataba mibovu itakwenda hivi, hakuna uwekezaji hapa. Ina maana tunataka kutoa mfumo wa kukandamiza taasisi zetu kuhakikisha watu wa nje wanakuja kuwekeza hapa na kuleta pollution. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikwenda Amerika ya Kusini; uwekezaji umepelekwa mkubwa sana Amerika ya Kusini; sasa hivi Amerika ya Kusini ni eneo ambalo lina pollution ya hali ya juu. Na Tanzania kwa mikataba mibovu tutakayoendelea nayo nina imani baada ya miaka mitano nchi hii itakuwa polluted yote; na mazingira yote mnayoyaona haya yatakwisha. Tujitambue na tusimamie kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na viwanda vya nguo zaidi ya kumi MUTEX, MWATEX, Urafiki, Sungura Textile, Tabora Textile na Riziki Textile, lakini viwanda vile vyote vimefungwa. Na katika kufungwa bahati nzuri Kamati ilitembelea EPZA, tukaenda kuangalia kiwanda ambacho kinatengeneza nguo za jeans, tukawauliza je mnapata wapi nyuzi? Wametujibu kuanzia sindano, uzi na kila kitu tunapata kutoka China. Tujiulize kweli tuko serious na uwekezaji? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naona ndugu yangu Mwijage wamekupa mzigo mzito kwa vile uliokuwa nao chini hawako serious kukusaidia, utakuwa unakimbia peke yako wataalam wako huku pembeni hawako serious na wewe kabisa. Haiwezekani tumefunga viwanda vya kusokota nyuzi, leo nyuzi zinatoka China, maana yake ni nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka uchumi endelevu, pana uchumi hapo? Wanawaajiri watu kwa miezi mitatu mitatu, Mtanzania huyo atapata faida gani hapa? Ina maana unamchukua miezi mitatu unamuachisha, miezi mitatu unamuachisha, hii nchi haiwezi kwenda katika mifumo ya namna hiyo ya mikataba mibovu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na viwanda vya kukamua mafuta; tulikuwa na Tanbond inatoka Tanzania, Super gee inatoka Tanzania, pride Tanzania na Mara ghee Tanzania; leo viwanda vyote mmefunga. Na wamevifunga tunaagizia blue band kutoka nchi za nje, are we serious? Halafu unapotaka kutuambia sisi tunakwenda katika mfumo wa viwanda vyote tumevifunga tunategemea vya nje hivi vina kasoro gani hata vimefungwa? Nenda Urafiki ni ma-godown, nenda Mtwara ni ma-godown, je, maendeleo haya mnayoyafanya mnayadumaza kwa makusudi halafu mnasema sasa hivi tunataka ulimwengu wa maendeleo ya viwanda, tutafika katika mfumo huo? Hatufiki, mikataba mibovu imefikia mahali ambapo sijui dawa yake ni nini, ni msiba kwa Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelewa na Shirika la Madini Tanzania (STAMICO), walikuwa na maeneo yao ya madini Tanzania nzima viwanda vya chumvi Lindi, Mtwara na Kigoma. Vile viwanda vyote vimefungwa na walipewa maeneo mengine kama ya uwekezaji ya Mererani. Mererani ina vitalu 29, STAMICO amepewa vitalu viwili tu. Mle ndani watu ni fujo tu na ndiyo maana unaona leo Tanzania tuna Tanzanite lakini inapelekwa nje ni kwa ajili tumesababisha njia za panya. Tunashindwa nini kuwauliza wale watu kwa nini wale watu wote wasishirikiane na STAMICO ili akaweze kupeleka uchumi, lakini imeshindikana yote ni kwa ajili ya mikataba mibovu. Tufike mahali tujiulize tunatakaje maendeleo ya uwekezaji na mikataba mibovu? Hii nchi imekuwa kaputi kabisa kwa ajili ya mitaba mibovu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepewa mradi wa uwekezaji na TANZAMOB ambao wamepewa na STAMICO; yule mwekezaji ni tapeli wa kutupa, ameanza kuchimba madini kwa muda toka mwaka 2011 anasema hajapata faida. Tujiulize, kwa nini hajapata faida na kwa nini anaendelea kuchimba? Miradi yote unayoiona Tanzania haina time frame, anafanya mtu biashara kwa miaka yotote anayotaka yeye. Sasa je, utasemaje tunaenda katika ulimwengu wa viwanda, ulimwengu wa uwekezaji tukiwa katika mfumo mbovu? Aibu. Tujiulize kweli nchi hii tunataka kuikwamua? Haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelea National Housing, mwekezaji Kawe alinunua majengo ya Kawe na heka 300 kwa milioni sita, milioni sita Watanzania nawaambia. Kawe ameinunua kwa milioni sita akalipa milioni mbili na laki tano, hakufanya chochote leo ameambiwa ana share na National Housing. Meneja wa National Housing anahangaika kutafuta fund yule anachukua hela ya bure na mapato ya bure, tutafika? Kwa mfumo huu tutafika? Kwa nyumba za bei rahisi mtazipata wapi? Huwezi kuzipata Tanzania anatozwa mpaka tozo la vifaa vya kuingiza kutoka nje kwa ajili ya ujenzi wa nyumba halafu unasema zile nyumba za bei rahisi, Mtanzania wa kawaida hawezi kukaa katika nyumba ya National Housing kwa vile mmeweka mikataba mibovu ya kumfanya National Housing asiendelee. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelewa na TANAPA. Kuna wawekezaji wako ndani ya Shirika la TANAPA ambao ni watu wa mahoteli, wake watu ni majambazi sugu ambao hawataki kulipa concession fee, halafu wanachokifanya ni kukimbilia mahakamani wakicheza na mahakama kuhakikisha TANAPA haipati tozo, mahakama iko chini ya nani? Matokeo yake sasa hivi tumeshashinda lakini bado wale watu hawataki kuona Waziri ambaye anafanya kazi wanasema tutamtoa kwa vile anatudhalilisha. Uchumi wa nchi umeshikiliwa na watu wachache ambao wamehakikisha nchi hii haiendi. Tunawajua, tunawafahamu na tunawafumbia macho.
Nchi hata kama mtafika mahali hapo kama hamsimamii sheria zetu, hamuangalii mikataba yetu nina imani kuwa hatutaweza kufika popote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelewa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (Tanzania Airport Authority); Tanzania tuna airport 58 amepewa airport nane tu; 50 zote zipo kwa watu wachache wanafanya shughuli zao huko, madini yanapotea huko, wanyama wanapotea huko na mali zinapotea huko ni kwa ajili ya mikataba mibovu. (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nikushukuru. Nimshukuru pia Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kunijalia kupata afya njema nami kuwepo hapa na kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile leo ni mara yangu ya kwanza, nitoe pole kwa familia ya Hayati Dkt. John Joseph Magufuli na Watanzania wote, kwa kweli nimeguswa na msiba wake na mimi ni mmojawapo wa wateule kwa nafasi ambayo nimekuwepo hapa Bungeni. Nitaendelea na kuwaomba Watanzania tuendelee kumwombea dua kwa vile alifanya mengi mazuri ambayo sasa hivi tunayaona, ili Mwenyezi Mungu amlaze na ailaze roho yake pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni Ujerumani na America wametoa pongezi kubwa kwa aliyepeleka research yake kule kuhusu suala la Corona, kwa kweli ile research yake dunia wameipongeza sana. Wanakuja kumpongeza sasa hivi Hayati ameshaondoka. Wakati ule anapambana walikuwa kama wanambeza kwa vile suala la Corona na mambo mengine ni biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nitaongelea suala la malaria. Mimi ni Mwenyekiti wa Kupambana na Malaria ndani ya Bunge. Kwa sasa hivi katika taarifa tulizokuwa nazo, kwa siku Watanzania 104 wanakufa kutokana na malaria. Ni gonjwa zito na kubwa na tishio kuliko hata Corona Virus. Kwa maana nyingine kwa mwezi Watanzania zaidi ya 3,000 wanakufa kwa ajili ya malaria. Sasa jiulize kwa nini sana wao wanatulazimisha tutumie hizi chanjo ya Corona wakati tunahangaika na kupambana na kutokomeza ugonjwa wa malaria. Zero malaria naanza na mimi, lakini kila Mtanzania nataka tuhakikishe tunapambana na tunatokomeza malaria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, malaria kuna mikoa sita ambayo ina maambukizo makubwa ya malaria; kwanza, Kigoma, Lindi, Mtwara, Ruvuma, Geita na Kagera. Na tumeambiwa tena Mkoa wa Geita utakuwa wa kwanza katika Tanzania kwakuwa na maambukizo makubwa ya malaria kwa ajili ya machimbo yaliyokuwepo kule Geita. Inamaana wachimbaji wanachimba, lakini hawaangalii athari zake kwa vile mikataba ya EIA (Environemt Impact Assessment) haikufanyika, hivyo watabakia jamaa zangu wasukuma kuwa ni wagonjwa ambukizi wakubwa wa malaria na watapata vifo vingi kwa kupitia katika machimbo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jiulize kama sisi tunakufa Tanzania ni nchi ya kumi katika nchi kumi na moja duniani ambayo inamalaria, maambukizi ya malaria makubwa sana mojawapo ni Tanzania, katika zile nchi kumi. Lakini sisi leo tunalazimishwa kufanya vaccination ya Corona, lakini hawajataka kutupa ufumbuzi, je, tutatokomezaje janga kubwa ambalo ni tishio kuliko hata Corona. Hapa lazima utajua kabisa hapa kuna biashara, zinaenda na hizi biashara tuziangalie kwa makini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeambiwa wanatangaza Tanzania tunapeleka dola milioni 45 kwa ajili ya kutokomeza malaria. Pesa zote zinazokuja za UKIMWI tunaziona katika Halmashauri na nyie Wabunge ni mashahidi hasa katika Local Government. Je, hizi hela za malaria zinakwenda wapi? Hizi hela zinakwenda kwa hao kutuletea dawa na vyandarua lakini hawana nia kabisa ya kutokomeza malaria kwa vile biashara zao ziendelee kufanyika ili na sisi tuwe wahanga wa vifo vya malaria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefungua kiwanda kikubwa Kibaha cha viuadudu wa malaria, lakini kwa vile wao wanafanyabiashara kile kiwanda kimeambiwa kuwa hakijakubaliwa na World Health Organization hivyo tumekaa na kiwanda ambacho ni kizuri nchi za wenzetu wanachukua dawa sisi tumeshindwa kutokomeza malaria wakati kiwanda kipo Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu, Mheshimiwa Waziri wewe ni pacha wangu, hakikisha halmashauri zote zinanunua dawa kwa kupitia, za kuua wadudu maambukizi kwa kupitia kiwanda cha Kibaha. Itakuwa ni dharau kubwa wanahela za ndani za kununua dawa hawanunui na hata wakinunua hawafanyi kazi hii ya kupulizia na kuhamasisha ili angalau tutokomeze hili janga la malaria. (Makofi)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Lulida kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Josephat Gwajima.

T A A R I F A

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge anaongea mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira. Tumetembelea hicho kiwanda cha hapo Kibaha ambacho kina utaalam wa ajabu, mzuri ambao haupo mahala popote Afrika Mashariki. Wacuba wametengeneza hicho kiwanda kwamba, wanatengeneza bacteria wanapowala hawa mbu, mbu wanakufa wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kusikitisha tulifika kwenye kiwanda hicho wafanyakazi wa hapo hawajalipwa miezi ya kutosha, wafanyakazi wanazunguka zunguka, kiwanda ambacho kingeondoa malaria kuna watu wanapambana nacho kwasababu malaria ikiondoka maana yake dawa za kupulizia zimeharibika, prescription za malaria hazipo. Kwa hiyo, namjulisha mjumbe kwamba anapambana na wafanyabiashara wanaopata fedha kupitia mradi wa malaria. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Riziki Lulida unaipokea taarifa hiyo.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli naipokea taarifa yake kwa vile yeye naye ni mzalendo kama mimi. Wazalendo kama Mr. Gwajima ni lazima tuwapongeze na nikubali maana yake kuna Wabunge wangetaka kutumika wakataka kukidharau lakini nimeona Mheshimiwa Gwajima ni champion na Mama Gwajima naye vilevile ni Champion kuhakikisha kuwa Tanzania bila malaria inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bima ya Afya, kama walivyozungumza Wabunge wenzangu ninamasikitiko makubwa sana na Bima ya Afya. Bima ya Afya haimlengi mtu na ni hii wazee zaidi ya miaka sitini, wazee wa miaka sitini ili atibiwe mahali popote inabidi atoe 936, tukiwemo humu Wabunge, Mbunge haruhusiwi kumtibu mzazi wake inabidi atumie mwenyewe kumtibu mzazi wake, sheria hii inatoka wapi? Na kama ipo naomba iletwe Bungeni tuibadilishe hii kanuni wazazi wetu nao wafaidike na matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta mzee anaumwa mimi nitoe laki tisa nimtibu mzee wangu wakati bima yangu mimi ni bima ambayo ni ya VIP. Lakini vilevile la pili, nataka Mama Gwajima unisikilize mara mbili mbili na hoja hii naileta. Hospitali ya Aghakan…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Lulida ngoja kwanza.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, haya.

NAIBU SPIKA: kwa sababu kina Gwajima wapo wengi sasa ukimwita Mama Gwajima hapa hatuelewi unamwita mama wa Askofu ama Mheshimiwa Waziri hapa. Kwa hiyo yeye mwite Mheshimiwa ili tutofautishe na kina Mama Gwajima.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, haya, Mheshimiwa Waziri, Waziri wa Afya, nataka nimwambie, Bima ya Afya katika hospitali kubwa ya Aghakan na Regency Hospital haiwataki wajawazito. Lakini ukichukulia malaria waathirika wa kwanza ni wajawazito na wanapeleka bima kule wanasema sisi hatupokei bima za afya za wajawazito. Je, ni maana moja wanawadharau wanawake na kama wanadharau wanawake, wanawake hatukubaliani nalo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wanawake ndiyo tunazaa Watoto, lakini leo unaambiwa pale hutakiwi kupewa nafasi ya kwenda kutibiwa kwa vile nini, utakuwa na gharama ya kwenda kupimwa pimwa mpaka kujifungua. Je, hii huoni kama inawakandamiza wanawake? na kulikuwa na haja gani ya kuwapa ruzuku mataasisi haya, wanaleta madawa na kila kitu wanapewa faida ya ruzuku lakini wanawakataa wanawake, tumeungana na wanawake Wenzangu wabunge wanataka uje utupe jibu kuhusu suala la Aghakan na Regency na vilevile waje watufanyie semina ya kututaarifu je, hizo hoja ni kweli na kama si kweli waje watuambie katika semina maalum hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Bima ya Afya ambayo tunakuwa nayo sasa hivi, ukienda Aghakan kama Mbunge tunalipa bima kubwa sana lakini tunakwenda kulazwa na watu wa kawaida wanaotoa shilingi 70 na kila kitu. Wanasema sisi hatuwezi kuwapa bima ya VIP lakini hii yote ni kutunyanyapaa na kutuweka katika mazingira magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba ukae na hizi taasisi ambazo zinachukua hela za walipa kodi watanzania na iwatendee haki watanzania kwa kuwapa haki sawa kwa wote. Wasijione wao wamekaa kule wanatoa gharama kubwa na kuwaacha wagonjwa wengine ambao wanahitaji bima za afya zao wanazitenga kutokana na wanavyotaka wao. Kama si hivyo, pelekeni Bima ya Afya Muhimbili, boresheni Muhimbili, tutakimbilia katika mahospitali yetu ambayo ni ya walala hoi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia changamoto za walemavu, walemavu ndiyo kundi maalum ambalo linahitaji msaada mkubwa sana katika tiba. Na katika tiba hizi hawa walemavu mpaka sasa hivi wanahangaika hawana Bima za Afya. Na kama hawana Bima za Afya hawa walemavu wengi wananyanyasika tu hawana mahali pa kukaa, hawana mahali pa kuishi. Lakini je, Bima ya Afya inasema nini kuwasaidia hawa kundi maalum ambao ni walemavu. Hatuna ma-desk ambayo yanasaidia walemavu hata katika mahospitali, leo anakwenda mlemavu ambaye ni kiziwi anataka kujifungua au ana matatizo lakini akienda pale hapati nafasi ya kusikilizwa, wanamchukulia kama mtu ambaye hana thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba hakikisha kuwa katika kila eneo la kituo cha afya, polisi ni lazima tuwe na desk maalum kwa ajili ya kusaidia kundi maalum la walemavu. Walemavu wanahitaji msaada wa kupata tiba kama watu wengine, walemavu wanahitaji kusaidiwa kama wengine, leo zinagawiwa chandarua Tanzania nzima lakini haimgusi mlemavu, kwa mara moja…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyenijalia kunipatia afya njema inayoniwezesha kuchangia katika hoja iliyokuwepo mezani. Napenda kukishukuru Chama cha Wananchi (CUF) kwa kuniona kuwa nina uwezo wa kulitumikia Taifa hili na kunipa nafasi ya Ubunge wa Viti Maalum na sasa hivi nipo katika Kambi ya Upinzani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kumshukuru Mheshimiwa Maalim Seif Shariff Hamad kwa juhudi zake anazozifanya, Mwenyezi Mungu atamjalia na atampa haki yake iliyokuwepo mezani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kunipa afya njema na leo nitajaribu kuchangia katika hoja iliyokuwa mezani hasa katika upande wa uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tuliingia katika uwekezaji kwa nguvu zote tukitegemea uwekezaji utatupa faraja kubwa na kuinua kipato cha nchi yetu. Tunazungumzia kipato cha 7.3%, lakini hiki ni kipato cha watu waliokuwa na uwezo wa hali ya juu. Ukienda kuangalia uhalisia huko vijijini watu ni maskini wa kupita kiasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia Tanzania tutaweza kukusanya mapato ya trilioni 14, hii ni pesa ndogo sana. Hizi pesa kuna wafanyabiashara sasa hivi wanazo, wameingia katika soko la dunia na kuonekana wao ni matajiri wakubwa, wana uwezo wa kuwa na trilioni 26, Serikali tukiwa na trilioni 14 kwa maana moja tumezongwa, tumekamatwa na wafanyabiashara wao ndio wataitawala nchi, hii Serikali itakuwa haina uwezo wa kuweza kujitambua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naingia katika uwekezaji, tumeingia katika uwekezaji lakini tulisema tulikuwa na malengo, goals, strategic, commitment, transparent, implementation, monitoring and evaluation, corruption, tumekwama wapi? Tafiti zote hizi zilifanywa na tukasema sasa hivi Tanzania uchumi wetu utakuwa mkubwa mpaka nchi nyingine kama Rwanda uchumi wao unakuwa kwa kasi sisi tupo nyuma pamoja na kuwa na resources zote ambazo tunazo. Tunataka tuseme kwamba tumekwama kwanza hatupo katika usimamizi uliokuwa bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, corruption imesimama kwa hali ya juu, baadhi ya viongozi wanaosaini mikataba wanaangalia matumbo yao, siyo kuangalia nchi inafanya nini. Usimamizi na ufuatiliaji wa miradi, Sekta ya Uwekezaji imeingia katika kila sekta kwa mfano, ukienda katika madini kuna uwekezaji bado hatujafanya vizuri; ukienda katika kilimo kuna uwekezaji, bado hatujafanya vizuri; ukienda katika viwanda na biashara kuna uwekezaji, bado hatujafanya vizuri; tumekwama wapi? Tusilizungumzie pato la asilimia 7, hakuna kitu hapo ni uchumi mdogo sana kwa Mtanzania na Watanzania tunakua, tunahitaji maendeleo, watoto wapate elimu na sisi wenyewe tuwe na maisha bora, lakini maisha bora kama hatujaweza kuangalia usimamizi huu tuliokuwa nao, tutakuwa maskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na suala la utalii, utalii unaingiza kipato cha nje (in forex), lakini leo utalii unaingiza asilimia 22.7, mianya ni mikubwa katika uwekezaji. Wawekezaji ambao wapo ndani ya utalii, ndani ya mbuga zetu hawataki kuchangia hata concession fee. Tunajiuliza usimamizi uko wapi? Kama wale watu wanapata nafasi yote, TANAPA inajenga barabara, Ngorongoro inajenga barabara na mazingira yote ya kuwapelekea maendeleo wale watu, lakini hakuna pesa wanazotoa. Matokeo yake tumekwama katika usimamizi, tungepata mapato makubwa kama tungekuwa tunasimamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Selous ambayo ni mbuga kubwa ya kwanza duniani, lakini haina kipato. Wawekezaji kule ni ujangili kwa kwenda mbele na hata hao watu wanaokamatwa, leo tunaona watu wanakamatwa na meno ya tembo 30,000, lakini hatujapata taarifa yoyote humu ndani ya Bunge. Mtu anakamatwa na pembe 30,000 ina maana ameua tembo 15,000 amefanywa nini, usimamizi upo wapi, mapato ya Taifa yapo wapi, tunaiacha nchi inaangamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwa na wanyamapori na misitu hakuna mapato yatakayopatikana ndani ya utalii. Utalii watu wanakuja kuangalia mazingira yetu tuliyokuwa nayo, iwe wanyama, na misitu yetu. Leo misitu inakatwa kama hatumo humu ndani, kuna Mtendaji wa Kijiji, kuna DC, kuna Mkuu wa Mkoa na watendaji wengine wanafanya nini kuhakikisha misitu inaimarishwa? Tembo atajificha wapi, faru atajificha wapi na simba atajificha wapi misitu yote inaangamia, mkaa kwa kwenda mbele, njia za panya zinaachwa, lakini viongozi wanahusika. Tunataka Serikali itupe tamko je, hali hii ya kuhakikisha utalii unakufa itaisha lini? Tunaona katika TV sasa hivi mpaka kobe, kasa wanatoka wanakwenda nje, sura pana wamekuja kuleta fujo ndani ya nchi hii, lakini tunawafanya nini sura pana? Hakuna.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji katika viwanda, wamechukua viwanda vyote wawekezaji vikiwemo Viwanda vya Korosho, Viwanda vya Mafuta, Viwanda vya Ngozi, lakini sijasikia viwanda vile kwa miaka 20 vikifanya kazi na Serikali ipo humu ndani, Mawaziri wapo humu ndani, watendaji wapo wanasimamia nini. Nenda Nachingwea kile kiwanda, ni ghala la kuweka mbao na majangili kuweka mapembe ndani ya vile viwanda, nani anafuatilia hivyo vitu? Nenda viwanda vya Mtama vya Korosho havifanyi kazi, Mtwara havifanyi kazi, Mbagala havifanyi kazi, halafu tunasema tunataka tupate uchumi endelevu, tutaupataje huo uchumi kama hakuna usimamizi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwe makini katika kusimamia, tufuatilie, tuachane na corruption. Corruption imekuwa ni donda ndugu ndani ya nchi hii. Hatujitambui, tumeachia uchumi tunaosema tuna uchumi, lakini uchumi huu ni kwa wageni, siyo Mtanzania halisia, nenda vijijini hakuna uchumi huo tunaozungumza hapa. Tusidanganye watu, tujipange katika uchumi ambao utamgusa mwananchi kijijini, siyo uchumi unawagusa watu waliopo Dar es Salaam na maghorofa. Maghorofa yale siyo ya Watanzania yale maghorofa ni ya wawekezaji ambao wanakwepa ushuru, wanakwepa kulipa kodi halafu tunajumuisha kuonekana Tanzania kuna uchumi wakati hakuna uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kuzungumzia suala la ajira na uwekezaji. Kwa vile hatusimamii humu ndani tumewahi kuuliza kwa Waziri, leo tunaona Wachina wanauza karanga Kariakoo, katika majumba ma-godown Wahindi wamejaa mle, wanatoka India kuja kufanya kazi za vibarua, je, Mtanzania atapata wapi ajira? Hakuna ajira kwa Watanzania, Watanzania hawana ajira, ina maana uchumi wa Tanzania unahamishwa kupelekwa kwa wageni. Tumejipanga kwa hilo, tunajiuliza maswali kama hayo kwa kujua, je, kama sisi Watanzania wazalendo tunajiangalia vipi. Tumeuhamisha uchumi tunaupeleka kwa wageni, lakini tumekaa hapa tunasema tunapanga mipango mipango, kila baada ya miaka mitano mipango, tunarudi nyuma katika enzi ya ujima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja katika upande wa kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo, lakini jiulize kila mwaka Tanzania kuna njaa. Hivi kweli kilimo kwanza kimemsaidia Mtanzania? Hakijamsaidia Mtanzania. Leo unampelekea Mtanzania kilo tano za mahindi, ana watoto, wajukuu, familia kubwa je, kilo tano alizopelekewa zitamsaidia nini Mtanzania yule?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefika mahali unajiuliza, mvua kama hivi sasa hivi ya kutosha ipo Serikali imetoa juhudi gani kuwapelekea wananchi pembejeo, Serikali imetumia juhudi gani kuwapelekea wananchi mbegu iwe za mahindi, ufuta au karanga, hakuna, lakini utasikia mwakani tunaomba msaada wa chakula. Hii inatokana na sababu kwamba, hamjazisimamia sekta ya kilimo, mnawafanya wananchi wanahangaika na hata pale anapoweza kulima, akapata mazao yake, hakuna soko kwa mkulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima ni kundi ambalo wamekuwa watu wa kutangatanga wakitafuta soko; inapofika wakati wa mazao, wanakuja wababaishaji kuja kuchukua mazao yao kwa bei ya kutupa. Mazao yale wanayapeleka nchi za kigeni kuwa kama raw material, nchi haifaidiki hata na mazao yetu. Tanzania hata mchele tunapeleka nje, tunaletewa michele mibovu, Tanzania tunatoa mbegu za alizeti, lakini tunaletewa mafuta mabovu kutoka Ulaya kwa nini. Ndiyo maana sasa hivi Tanzania tuna kasi kubwa ya kansa, tunakula mafuta mabovu, lakini je, viwanda vyetu vinafanya nini, tulikuwa na viwanda vya kusindika mbegu na kupata mafuta Mwanza…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Lulida muda wako umekwisha.
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye amenijalia kuwepo leo na kuweza kuchangia katika hoja hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu amjalie Maalim Seif Sharif Hamad kipenzi cha Watanzania hasa Wazanzibar ambao walijitahidi kumpatia kura za ndiyo lakini Mwenyezi Mungu anasema walatazidu-dhwalimiina ila hasara. Imetendeka hasara kubwa na dhuluma kubwa lakini mwenye kuwa na kiburi duniani hapa ni Mwenyezi Mungu peke yake alaysallah bi-ahkami-l-haqimiina. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nataka nizungumzie suala la ajira. Uchumi wa Tanzania umechukuliwa na wageni, wageni wameuchukua uchumi wetu kwa kupitia ajira za Tanzania. Sasa hivi ukiingia katika viwanda vyetu ambavyo viko katika Manispaa wafanyakazi walioko mle ndani wengi ni wageni na wametengeneza maukuta mtu yeyote hata mfanyakazi anayetoka Wizara ya Kazi hawezi kuingia mle. Maana yake ni kuwa uchumi ukipelekwa kwa wageni Watanzania watabakia kuwa ni maskini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mfano, Dangote ameanzisha kiwanda Mtwara lakini mpaka sasa hivi wamegundulika wafanyakazi 360 kutoka nje ambao hawana vibali. Kwa maana hiyo, wananchi au Watanzania ambao wanahitaji kupata kazi pale hawana nafasi lakini nafasi hizo zimechukuliwa hasa na sura pana. Tujiulize, hawa sura pana ndani ya nchi hii wamekuwa kama panya ndani ya ghala, wanakula karanga wanatubakishia maganda na nitaitolea ufafanuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri zetu hasa za Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma ambazo tunalima korosho sasa hivi sura pana wanakwenda kununua mazao ndani ya vijiji. Huu ni uhuru ambao hauna mipaka. Kule vijijini wanakokwenda wanafanya kazi nyingi sana. Kwanza, wanasema wananunua korosho, ufuta lakini kazi kubwa wanayoifanya kule ni uwindaji haramu. Sasa hivi tunaona misitu imekwisha, tembo wamekwisha, tujiulize wako hapa kutusaidia au wamekuja kutuharibia uchumi wa nchi yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini napata kigugumizi sana, tunaona watu wanawasifia, jamani hatujioni kama tunateketea? Tuko katika uchumi mgumu tunahakikisha kila kinachopatikana kinakwenda kwa wageni. Tufike mahali tujiulize tutakaa lini tujitambue, tuache uzembe ili tuangalie hawa sura pana wapo kutusaidia au wamekuja hapa kutumalizia uchumi wetu? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia suala la zao ya korosho katika Mikoa ya Kusini. Tuna export levy zinapatikana zaidi ya bilioni 30, hizi pesa hazijulikani zinakwenda wapi. Tulitegemea hizi pesa zikafanye kazi ya kutengeneza madawati, kununua dawa, ni ulaji ambao hauna mipaka ndani ya mikoa hiyo. Naomba tusimamie hela za export levy tuzijue zinakwenda wapi maana zimeliwa kwa miaka mingi mpaka sasa hivi haijulikani kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, Mkoa wa Mtwara wana export levy, katika hela hizo 60% zinakwenda kwa Mkuu wa Mkoa anazitumia kwa kitu gani? Hakuna madawati, dawa…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Lulida nilikupa dakika tano na zimekwisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru na mimi kupata nafasi hii ya kuchangia katika Wizara ya Maliasili na Utalii. Mimi ni-declare interest kwamba ni mdau wa maliasili. Kwanza nimezaliwa Selous, lakini ya pili ni Mwenyekiti wa Kupambana na Ujangili, say no to poaching. Bahati nzuri Kamati yangu tulizunguka Tanzania nzima, tukaona mazingira ambayo tumeyaona lakini nataka na mimi nitoe kama ushauri kama utaweza kusikilizwa, lakini tuangalie suala la uhifadhi na environment ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata bahati kuhudhuria mikutano mbalimbali ya climate change. Tanzania sasa hivi tunakwenda kwenye gold, tumetoka katika green tunakwenda kwenye gold, maana yake Tanzania inakwenda kwenye jangwa. Sasa tujiulize tunaangalia maslahi ya nchi au tunaangalia maslahi binafsi ya kwamba mimi niwe Mbunge, ili fujo ya nchi kuingia katika disaster ya kuwa katika gold na hali ya nchi kuwa katika ukame. Wabunge sisi tujiulize na tujipe nafasi ninachokizungumza nchi yangu inakwenda wapi? Tunakwenda katika jangwa! Tulikuwa na Profesa mmoja akatuambia mnaiona Tanzania? Tanzania inakwenda katika jangwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nchi za Uarabuni wanapanda miti na kuhakikisha wanautoa udongo India, kuhakikisha Arabuni kama Dubai inakuwa katika green na mvua wanapata sasa hivi. Lakini Tanzania mito mingi mikubwa sasa hivi inakauka na inapotea kabisa. Nataka nimshukuru na niwapongeze watu wa Ngorongoro, niwapongeze watu wa TANAPA na Wamasai waliopo ndani ya Ngorongoro, wale ni wahifadhi wazuri na wanasimamia ndiyo maana mpaka leo Ngorongoro Conservation inaonekana kama Ngorongoro Conservation. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonekana TANAPA na uhifadhi wake, na kutoa tozo kubwa kwa ajili ya Serikali mwaka huu wametoa shilingi bilioni 10. Niko katika kamati ya uwekezaji, mashirika ambayo yameweza kujitegemea ni Ngorongoro, TANAPA, National Housing na TRA basi, mashirika mengine yote yako katika hali ya kufa. Sasa tujiulize tunataka uhifadhi au tunataka tuhakikishe uhifadhi hamna, mvua hamna tutaishije Tanzania hii? Hata mito haitakuwepo. Leo wewe ni mfugaji unaingia ndani ya Pori la Serengeti kuna simba, kuna tembo mgongoni una bunduki, nipe tafsiri yake ni nini hapo? Sielewi kabisa hiyo picha inayoniambia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu pili tuhakikishe haya mapori ni michoro ambayo ilikuwepo tangu enzi ya mkoloni, walijua tuwaweke maeneo ya uhifadhi hawa Waafrika watamaliza misitu yote watahakikisha hifadhi hakuna hata mvua itakuwa haipatikani. Na ndiyo maana kuna demarcation kuna, kuna ma-beacon ambayo yameweka mle ndani kuhakikisha hizi alama zinaendelea kudumu lakini kwa uhifadhi waliamua kuhakikisha wamewagawia, mwisho tunajiuliza je, tugawe hifadhi zote watu wachukue wamalize wafugaji halafu hii nchi ikae katika ukame? (Makofi)
Nataka nitoe tafsiri ya hili, wafugaji walipelekwa Mkoa wa Lindi walitoka Ihefu, Ihefu ilikauka kabisa TANESCO hata mvua ilikuwa hamna, maji hamna nchi ikaingia katika giza. Lile giza limepelekwa Lindi, shamba la bibi Lindi nenda leo Selous hakuna simba, nenda leo Selous hakuna ndovu wamehakikisha wafugaji wameingia mpaka ndani ya Selous.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tujiulize tunaangalia maslahi ya nchi au tunaangalia mimi nichaguliwe kuwa Mbunge halafu baadaye niendelee kuwa Mbunge nchi iingie katika disaster haikubaliki. Ninakuomba Waziri mwenye dhamana toa semina Wabunge wajitambua kama uhifadhi ni kitu kizuri ndani ya nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwaka 2008 nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya Maliasili Mwenyekiti wangu alikuwa Job Ndugai. Ni wewe ndiwe uliyeanzisha CNN, ndipo Tanzania ikaanza kukua katika utalii. Ni wewe ndiye ulileta fixed rate watu wakaambiwa ni lazima watu wenye mahoteli walipe baada ya kuona wewe unataka kuupaisha uchumi na wao kazi yao ni kuuhujumu uchumi walikuondoa kwa kuhakikisha uchumi ulio ndani ya maliasili unaporomoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuombea kwa Mwenyezi Mungu akulinde, akupe afya njema uiongoze nchi kama anavyoiongoza Waziri wa Ardhi na wewe nataka nikupe fimbo hiyo ufanye kazi hiyo, kazi kwa kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimezaliwa Selous, nimezaliwa Selous mimi ni Mngindo kwa asili ninatoka ndani ya Liwale. Selous ndiyo mbuga kubwa ya kwanza katika Afrika na ninaweza kusema ni duniani haijatangazwa, kuna corridor kubwa ya tembo ambao wanatoka Mozambique wanakuja Tanzania wakiingia Tanzania wanaingia Namtumbo, wanaingia Masasi, wanaingia Nachingwea, wanaingia Liwale, wanaingia Kilwa wanakwenda mpaka Mahenge wanavuka wanakwenda mpaka Tarangire. (Makofi)
Sasa ushoroba huu wanafaidika nini na watu wa Kusini? Ninaomba madawati yaliyopangwa ya TANAPA yawapeleke watu wa Lindi, Mtwara na Ruvuma wafaidike nayo. Huyu sungura asigawiwe kwa upande mmoja, hii siyo haki. Tulidai haki ya gesi mkasema gesi ni ya Watanzania kwa nini madawati mnagawa kwa mafungu? Nataka nihakikishiwe, Mheshimiwa Waziri pamoja na kukupenda sana kama haujapeleka allocation Lindi sitakubaliana, kama hujapeleka allocation Ruvuma sijakubaliana na wewe na kama hujapeleka allocation Mtwara kwa kweli sikubaliani nawe na ninaomba sheria hii irudishwe hapa tuifute ili angalau Tanzania nzima wafaidike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Lindi unaongoza kuwa na rasilimali kubwa, tumepiga kelele ya mjusi ambaye yuko Ujerumani kila mwaka wanapata dola bilioni tatu Tanzania hata senti tano hatuipati. Hapa wanatufanyia dhihaka mjusi, mjusi, lakini ni haki ya mjusi. Maeneo yale tupate shule, tupate barabara lakini mpaka leo watu wa Ujerumani wanafaidika na yule mjusi, sisi tunapata nini? Nataka Mheshimiwa Waziri wa dhamana aniambie tozo linalopatikana kutokana na yule mjusi linakwenda Mipingo Tendeguru, sisi tusibakie kama boga linasuka mikeka wenye tunalala chini, hatukubali kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kilwa iko katika urithi wa dunia na katika urithi wa dunia Kilwa ni namba 21 duniani hata hizo Ngorongoro, TANAPA ziko nyuma lakini kwa vile iko Kusini mpaka leo imeachwa katika urithi wa dunia. Hautuzwi, hakuna mapato, hakuna kinachoangaliwa kule Kilwa zaidi ya tumepaacha hakuna ndege zinazokwenda kule, watu wanakwenda kinyemela nyemela hakuna mapato yanayopatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la utalii. Mtalii akija Tanzania anakuja na package, anaingia TANAPA, anaingia Ngorongoro, anakwenda Zanzibar. Masikitiko yangu makubwa Zanzibar hakieleweki hela zinakwenda wapi? Imefikia mahali kuwa tozo zinazopatikana Zanzibar ni hela za watu wajanja, inafikia kujiuliza Zanzibar kuna nini? Utalii wa Sychelles umewafanya mkawa matajiri, Zanzibar watu wanaendela kuwa maskini kwa vile hawasimamii rasilimali yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Zanzibar wameshindwa kusimamia utalii tupo tayari kusimamia utalii wa Zanzibar na utaruka. Kama huku TANAPA wanaweza kukusanya shilingi bilioni 100, Ngorongoro shilingi bilioni mia moja na Zanzibar iko wapi hela ya utalii aibu kubwa sana. Ifike mahali ujiulize kuna fanyika nini mpaka Zanzibar ikaonekana hata utalii wa maana, pesa inayongia kama concession fee Zanzibar hakuna? Kule kuna ujanja na ulaji ambao hauna mwenyewe na kazi yao kutoa vitenge, wakiwapa vitenge wamemalizika tuuangalie utalii wa Zanzibar kwa jicho la huruma watu hawa waweze kusaidiwa.
Na wampe Maalim Self afanye kazi
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru na nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia afya njema na niwaombee Mwenyezi Mungu vilevile awajalie Wabunge wenzangu wapate afya njema tuweze kulitumikia Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanzia na mazao mchanganyiko hasa katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani. Watu wa Mikoa ya Kusini walikuwa wanategemea mazao mchanganyiko kama ufuta, korosho, kunde na mbaazi. Katika nchi hii ya Tanzania tuligawanyika katika baadhi ya mazao yanayotokana na maeneo fulani, nasikitika sana tuliwaacha wafanyabiashara wachache wanaiyumbisha nchi kwa kununua mazao kwa bei ya chini na kuwafanya wananchi kuwa maskini. Tujiulize wataendelea wao kujitangaza matajiri mpaka lini, wananchi wa Kusini na Watanzania wanaendelea kuwa maskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, leo katika soko la Euro wanauza ufuta kilo moja euro tatu na wafanyabiashara hawa wanachukua ufuta Lindi, Mtwara, Pwani wanaupeleka Sri Lanka, ina maana ajira inakwenda Sri Lanka. Tunawaona hatuwaoni? Lakini tumenyamaza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshindwa kutafuta soko kwa wananchi kuweza kuwakwamua leo ufuta kutoka 3,500 wananunua ufuta kwa shilingi 600 mpaka shilingi 800 na wengine upo majumbani hawana pa kuupeleka kwa ajili ya hawa wafanyabiashara wanaiyumbisha Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tujiulize kwa miaka 50 kwa nini tumeachia uchumi wetu unachezewa na kukanyagwa kanyagwa na watu wachache. Ni hali ambayo imetufanya wananchi wamedhoofika, wananchi wamekuwa maskini kwa kuwa wafanyabiashara wanajiona wanakuwa matajiri na kuwaacha wananchi wanaendelea kuwa wanyonge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaazi zipo majumbani kutoka shilingi 3,800 mpaka shilingi 800 hazitoki, kunde, njugu na choroko zipo majumbani wao wameukamata uchumi na uchumi huo wameukamata kwa vile wana mahali wanapoegemea, wajiulize kwa nini wanaendelea kuikandamiza nchi ya Tanzania na Watanzania wenyewe wenye ngozi nyeusi wakiwa maskini, tujiulize tunajitambua Watanzania? Hatujitambui. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda muafaka kila Mtanzania humu ndani ajione kuwa yeye ni part and parcel ya kutetea wanyonge wa Tanzania. Watanzania wanadhalilika, mama lishe anakimbizwa Tanzania nzima kwa ajili ya kuambiwa atoe kodi lakini kuna ma-giant hawalipi kodi. Wanatufanya Watanzania kama sleeping giant ambapo wao hawatozwi kodi na wameamua kulindwa, Serikali kama inataka kusema kweli iwashughulikie hawa watu, haina haja ya kuwasema humu ndani mnawatambua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Lindi, Mtwara na Pwani tulikuwa na viwanda vya korosho 13 vyote havifanyi kazi. Lindi peke yake haina ajira ya vijana hata moja kwa vile viwanda vyote vimefungwa. Je, tutawapelekaje vijana wale ambao hawana ajira watafanya kazi gani, wamelima ufuta, wamechukua mikopo benki, lakini leo ule ufuta uko majumbani. Hao vijana tunawapeleka wapi?
Tunataka tuhakikishe uchumi wetu utakwenda wapi, watoto watasomaje katika mfumo ambao unaona kabisa ni kandamizi wao wanatangaza mimi nitakuwa tajiri wa dunia, halafu hawa watu wa chini wanakwenda wapi? Ni kitu cha aibu, inabidi Watanzania tujiulize tutaendelea kuwalinda mpaka lini? Mimi na wewe wote tunataka tuangalie wananchi wanyonge wanapata haki yao, haki sawa kwa wote na asiependa haki aelimishwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri Serikali imesahau uwekezaji hasa katika mabenki, yameingia mabenki mengi utitiri, riba zinatofautiana lakini anayekandamizwa mwalimu, daktari, mbunge, nesi na watu ambao wanachukuwa mikopo katika mabenki. Wao wanategemea taasisi zetu kuenda kuweka fixed deposit katika mabenki yao, mikataba wanayowekeana ni kutoka asilimia nne mpaka nane lakini leo mabenki wanatutoza riba ya asilimia 18.5 na kuendelea. Je, mwalimu wa kawaida ataweza kudumu au ataweza kumudu uchumi wa namna hiyo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tujiulize kwa nini wanaweka riba kubwa jibu halipatikani. Leo kila mwezi wanakukata kodi, unakatwa kodi katika mshahara, unakwenda benki unakatwa kodi na bado unaendelea kuweka riba kubwa mara mia tatu mpaka mara mia nne tunasema nini humu ndani kuhusu watu hao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, benki ni mwiba, leo ndani ya benki tunasikia lakini hakuna anayeguswa kwa vile ndani mle hakuna Lugumi wala hamna UDA. Lakini angekuwepo UDA humu ndani mngesikia kelele Bunge zima humu ndani. Wanatuibia vya kutisha, ukiweka pesa benki ukikaa mwaka mmoja haujaigusa akaunti yako hamna pesa mle ndani ya benki, tunafanya nini na riba chafu kama hizi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata katika Qurani wamesema riba ni haramu, lakini tunaona kabisa riba ni kubwa na zinawakandamiza Watanzania hatuangalii ndio maana wanajiuliza kwa nini sasa hivi wanaanza kupata woga, wanapata woga kwa vile walizoea kufanya wizi wa kukithiri ndani ya mabenki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, benki zetu zimekuwa siyo rafiki kwa Watanzania, anakopa Mtanzania anawekewa riba kubwa ambayo anashindwa hata kuimudu, ndiyo maana leo hata akina mama lishe wakikopa pesa benki ananyang„anywa vitanda vyake, magodoro yake maana yake wao wanaweka vitu vya vidogo vidogo kutokana na uwezo wao.
Naiomba Serikali iiangalie hii riba katika mabenki ni wizi wa aina yake. Na kwa nini sasa hivi wanajaribu kukimbiakimbia kusema wanataka kufunga, huu ni uongo! Watu wa benki wamecheza michezo michafu kwa muda mrefu sasa hivi wanajaribu kusimamiwa ndiyo maana wanasema tunafunga benki, lakini hawafungi benki ni kwa ajili ya wizi waliouona ni mkubwa ambao unawakandamiza Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaingia sasa hivi katika mbunga yetu ya wanyama ya Selous Game Reserve sitaki kuangalia sehemu nyingine yoyote. Nimeizungumzia hii mbuga zaidi ya miaka kumi ndani ya Bunge hili. Selous Game Reserve ni mbunga ya kwanza kwa ukubwa duniani, lakini ndani ya Selous sasa hivi watu wanachimba madini. Tunachimba uranium, wanachimba dhahabu, wanachimba almasi sisi wenyewe tupo hapa humu ndani? Nani atatuletea ufafanuzi kuwa ndani ya Selous kunafanyika nini? Hakuna kinachojulikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wameifanya Selous kama shamba la bibi, mapato ya Selous tungeweze kuhakikisha yanawasaidia Watanzania wengi na wanyonge wakafaidika hata na ajira. Lakini ndani ya Selous sasa hivi hakuna kinachoendelea zaidi ya kuchimba madini mengi yako mle ndani, kuhakikisha msitu wote unakwisha, wanyama waliokuwa ndani ya Selous wamekwisha. Je, tunakwenda wapi na uchumi wetu? Tufike mahali tujiulize Tanzania, hivi kweli tunaitakia mema nchi hii?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wachache ambao wanaingalia Tanzania kwa huruma, watu wengi hawataki kuangalia kwa huruma na ndiyo maana mpaka leo meno ya tembo yanauzwa na tunayaacha hivi tunaangaliana. Kila siku tunaangalia meno yanaondoka, kutakuwa na tembo nchi hii, kutakuwa na utalii nchi hii? Na utalii peke yake unatuingizia 27.5 percent, lakini unaona Selous imetupwa haina ajira haina kazi wala kinachofanyika ndani ya Selous; haiwezekani hali imefikia mbaya sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kuangalia hali tete inayohusu mazao. Tufike mahali tuwaonee huruma wananchi, wakulima wanalima, mpaka leo mazao yao yamekaa ndani hawajui yatayauza wapi? Leo ufuta kutoka shilingi ngapi wamekaa nao ndani mpaka shilingi 800 hakuna soko la ufuta. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshindwa kutafuta soko la ufuta, tumefika mahali wananchi tumewakandamiza hata pa kupita hawajui, wamekaa wamechanganikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike mahali, Serikali iangalie kwa makini mabenki na wakulima wanaokopa katika mabenki wanadhurumika vibaya mno. Mabenki yanaweka riba kubwa na ndiyo maana sasa hivi wanajidai ooh tumefilisika, hawajafilisika hawa, wanabadilisha majina tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na nimshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia afya njema na kuwepo katika kuchangia hii hoja ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe pole kwa familia ya Mheshimiwa Dkt. Macha ambaye Mwenyezi Mungu amempenda zaidi. Kwa muda mfupi niliokaa na Mheshimiwa Dkt. Macha nimejifunza vitu vingi sana na nikikaa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu huwa nawaambia
Mama Macha alikuwa na kipaji maalum kwa walemavu hasa. Hivyo Mwenyezi Mungu amrehemu amuweke katika njia iliyokuwa sahihi na ampe pepo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, napenda nitoe pongezi za dhati kwa Waziri Mkuu, Waziri Mkuu ni mtu mnyenyekevu, huruma, na mwenye upole. Nataka nimpe usia mmoja kama ndugu yangu, tulichukua Qurani na Biblia tukasema tutatenda haki kwa Watanzania. Nina imani kwa unyenyekevu na upole wake atawatendea haki Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania sasa hivi tunasimama kutaka kutatua migogoro ya Burundi, tunaiacha Zanzibar iko katika mgogoro, Zanzibar ni mwiba. Mwiba ule kwa unyenyekevu kabisa, nakuomba Waziri Mkuu uliapa kutenda haki na kuwatetea Watanzania, basi lile unaloliona wewe litakuwa haki ulisimamie kwa vile Qurani hii itakuja kutuadhibu siku moja. Qurani na Biblia zetu hizi zitakuja kutuadhibu siku moja tutende haki kwa waislam, wakristo
na wote wanaopenda haki katika Tanzania hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo, nataka nimshukuru tena Waziri Mkuu, nilitoa hoja ya kumuomba Waziri Mkuu ashughulikie suala la korosho kuhusiana na tozo. Napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu nikiwakilisha wananchi wa Mtwara, Lindi na walima
korosho wote kwamba ameweza kulitatua tatizo lile kwa asilimia kubwa sana, sasa hivi tuko katika neema. Neema hii tunaomba iende katika mazao ya tumbaku, pamba na kahawa. Naamini Mheshimiwa Waziri Mkuu una uwezo mkubwa, ahsante sana na Mwenyezi Mungu atakujalia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka katika Mkoa wa Lindi. Mkoa wa Lindi ni wa mwisho katika maendeleo lakini ni wa kwanza kwa kuwa na resource nzuri, lakini bado keki ya kugawiwa Lindi inapelekwa ndogo sana. Nataka niongelee tatizo la maji Lindi na ni karibu miaka 10 tunazungumzia, leo Manispaa ya Lindi imetumia shilingi bilioni 51 lakini hakuna maji. Hata hivyo, nataka nitoe sababu ya msingi inayosababisha miradi ya maji kufeli. Tunawapa
wakandarasi kutoka India na hela zinapelekwa shilingi bilioni 51, mkopo wa Watanzania, mkopo wa walipa kodi, kwa nini zipelekwe India? Tunaagalia mradi wa maji wa Chalinze,
shilingi bilioni 51 hela zote kunapelekwa katika Benki ya India sio Bank of Tanzania. Tujiulize, maji hakuna tayari mabilioni yanakwenda India, kwa faida ya nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu ana meno na macho ya kuangalia, nashauri akaangalie hili suala la maji Tanzania nzima. Kila ukija humu ndani watu wanalalamikia maji lakini mabilioni ya pesa ya maji yamepotea kwa ajili ya wazembe wachache ambao wamefanya wanawake wanatoboka utosi kwa ajili ya kutafuta maji kisa wao wananufaika na kuzichukua zile pesa kuzipeleka India. Inakuwaje mkopo wa World Bank unachukua pesa za Mtanzania, zinawekwa Benki ya India na sisi wenyewe tumenyamaza? Cha kushangaza miradi hii yote wamepewa Wahindi, kuna syndicate hapa. Naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kabla hujamaliza kuhitimisha uandae Tume ujiulize ni akaunti ngapi za maji zimepelekwa nje? Akaunti ngapi za ujenzi wa barabara zimepelekwa nje na kwa faida ya nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji wa Lindi mpaka leo haujafika hata shilingi bilioni mbili lakini tayari shilingi bilioni 51, nilikuwa Mjumbe wa Bodi ya Maji, alipewa MS Jandu shilingi bilioni 13.7 maji hayakupatikana Lindi. Akapewa tena shilingi bilioni 16 maji hayakupatikana Lindi. Amepewa shilingi bilioni 29 maji Lindi hamna. Je, hizi hela za walipa kodi tunazifanya nini? Ni madeni ambayo yangeweza kuzuilika lakini haiwezekani kutokana na watu wachache wanaifanya hii nchi isitawalike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya ya kusimamia uhifadhi wa wanyamapori. Mimi ni mdau wa wanyamapori, ni Mwenyekiti wa Kupambana na Ujangili. Kwa idhini yako, nataka nimuombe ahakikishe mpaka wa Gorogonja ambao unaunganisha Serengeti na Masai Mara usifunguliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri Waheshimiwa Wabunge wengi hawaelewi ni wapya, nashauri wapewe semina wajue kwa nini mpaka wa Gorogonja usifunguliwe. Mtalii akija Tanzania atarudi kwenda kulala Kenya, uchumi wote utapelekwa Kenya. Ni lazima tuhakikishe kuwa tunajitambua kuwa ule mpaka ni sumu kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na mzigo muda mrefu nataka niutue, lakini leo nataka nimtulie Waziri Mkuu mzigo huu. Mjusi ameanza na Mheshimiwa Mudhihir akashindwa mahali pa kuupeleka yule mjusi. Akaja Mheshimiwa Mama Mikidadi na Mheshimiwa Riziki, dinosaur
ambaye yuko Ujerumani nimeshindwa kulitua. Hapa simtulii Mnyamwezi wala Mndengereko mzigo huu namtulia Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato yanayopatikana na dinosaur yule ni makubwa sio ya kubeza ndani ya Bunge hili. Leo watu wa Lindi hatuna mirahaba ya TANAPA, hatupati tozo yoyote ya Ngorongoro lakini tungepata pato la mjusi, shule za Mipingo, Matakwa, Namapwia, tungepata
barabara, tunajiuliza kigugumizi kiko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nasema tena, sitamuuliza swali hili Mheshimiwa Maghembe, nitauliza Ofisi ya Waziri Mkuu mpaka Mwenyezi Mungu aniondoe katika Bunge hili, suala la mjusi limefikia wapi? Naomba suala la mjusi huyu ulipokee wewe na unijibu wewe siyo mtu mwingine tena. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja tena katika masuala ya uwiano wa maendeleo katika Mikoa ya Kusini, Lindi na Mtwara. Mradi ambao ni mwiba katika Mkoa wa Lindi ni huu Mradi wa TASAF. Bahati nzuri nilimpelekea document kuonesha shule zilizojengwa Lindi ziko chini ya viwango,
hospitali zilizojengwa Lindi ziko chini ya viwango, vyoo vilivyojengwa Lindi viko chini ya viwango, maji yaliyopelekwa Lindi hayapatikani, yote ilikuwa ni miradi ya TASAF, lakini nataka nitoe sababu na yeye kwa vile yuko humu ndani akalisimamie, tuko pamoja kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya viongozi wamekuwa miungu watu ndani ya Wilaya zetu, hawa wanaitwa Makatibu na Wenyeviti. Wale wanawatisha Madiwani wasifanye kazi zao, wasikague miradi, matokeo yake nafikiri umeona. Choo cha TASAF kimejengwa kwa
karibu shilingi milioni 100 hakuna choo. Darasa limejengwa limeshaanguka. Je, tutaendelea na TASAF III wakati TASAFI… Kuhusu Utaratibu....
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniongezee muda wangu. Mheshimiwa Waziri Mkuu mjusi namhamisha kutoka kwa Mheshimiwa Riziki, Mheshimiwa Bobali, nakukabidhi tupate mapato na tozo liende Namapwiya, Mipingo na Nangaro. Wakati Mheshimiwa Rais anakuja Nangaro alisema atatuletea mapato katika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema nashukuru na nawapenda Watanzania wote, Mungu ibariki Tanzania na Mungu mbariki Waziri Mkuu. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru kwa kunipa tena nafasi hii. Naitwa Riziki Said Lulida, Mama Tembo, Mama Mjusi, Mama Selous na ni Balozi wa Utalii. Nataka niwapongeze kwa dhati katika Wizara ya Maliasili ikiongozwa na Waziri na Naibu Waziri. Pia kuna watu wamefanya kazi kubwa ya kusimamia utalii na maendeleo ya wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitawataja kwa majina; kwanza inaongozwa na Mheshimiwa Ndugu Allan Kijazi. Kwa kweli amefanya kazi kubwa. Mheshimiwa Fred Manongi wa Ngorongoro, mpaka wanazeekea ndani ya utalii na kuweka heshima kubwa ya nchi hii. Wamefanya kazi kubwa. Bwana Silayo Dosantos katika TFS, mmeona hata mapato ya misitu yamekuwa makubwa na bila kusahau na wahifadhi wengine ambao wana upendo, ikiwemo sisi Wabunge ambao ni Ma- champion wa kupenda maendeleo ya utalii ndani ya nchi hii. Tanzania ili tuendelee tunahitaji mapato ambayo yataisaidia nchi hii.

Katika upande wa maliasili ya Tanzania watalii wanakuja kwa ajili ya masuala ya wanyama watano tu, big five ambao ni Simba, Tembo, Nyati, Chui na Faru. Bila hivyo, kuwahifadhi hawa wanyama, basi hatutaweza kufanikiwa, tutarudi nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie wenzetu Kenya, Masai Mara ni eneo dogo sana, lakini wamefanya kazi kubwa sana ya kutangaza utalii kwa kupitia Masai Mara. Sasa nataka nami niwasaidie vile vile tuweze kufanya kazi ili tuweze kupata pato kubwa, kumsaidia Mheshimiwa Mama Samia Suluhu katika eneo hili la utalii, kama alivyokuwa champion kuhakikisha kuwa Tanzania yenye mapato ya ndani kupitia Hifadhi zetu pamoja na maliasili yetu inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo hayo ni kama ifuatayo: kama alivyozungumza ndugu yangu Kanyasu, kwa kupitia International Conferences na Global Summit kule ndiyo watu wanakwenda. Niulize TANAPA imewahi kwenda katika mikutano kama hiyo? Hawana Fund. Ujiulize Ngorongoro wanatangaza maeneo kama hayo? Hakuna. Hivyo lazima tutarudi nyuma na wenzetu wanatupita kwa ajili ya kutangaza na kuhakikisha matangazo yao/promotion zao na marketing zinakuwa kubwa na ndiyo maana unaona tunapitwa mpaka na Masai Mara ndogo kama ni wilaya tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwa kupitia airlines; leo ingia katika KLM unaiona Kenya inatangaza, come to Kenya and visit Serengeti, Ngorongoro and Zanzibar. Sasa unajiuliza, tunakwenda wapi? Kwa nini wamefikia pale? Ni kwa sababu wanatangaza matangazo makubwa sana ya kidunia na ndiyo maana mapato yanapatikana. Kwa kupitia ma-tour operators, wengi wanakwenda, mimi nimewahi kutembea nao, lakini ni wachache. Wengi hawafanyi kazi ya kutosha. Kama wangefanya kazi ya kutosha, Tanzania hii ambayo tuna mbuga nyingi, tumeambiwa sasa hivi TANAPA wana 22. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tungekuwa tumezipita nchi za Afrika zote kwa mapato, lakini kwa vile bado hatujajitangaza inabidi tufanye kazi kubwa ya utalii wa ndani. Tufanye kazi kubwa; na Watanzania hata Wabunge humu ndani; kuna Mbunge mwingine ukimwita unakujua Serengeti? Atakwambia mimi sikujui. Tulete mafunzo ya kutosha, tutembee nao Wabunge hawa wakaone haya yanayozungumzwa. Mimi ni Mwenyekiti wa kupambana na ujangili ndani ya Bunge; nimetembelea mbuga, ndiyo maana nimeiokoa Mbuga ya Burigi, imerudi katika Hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanyamapori inabidi walindwe, lakini na wafugaji wanaingia ndani ya mapori wakiwa na ma-rifles na mabunduki makubwa sana. Wengi wao wanakwenda kibiashara na katika uindaji haramu. Kupitia mimi, nimekwenda pale kwa kuwa nimenyanyaswa kwa vile ni mfugaji, haikubaliki. Mimi naikataa hiyo. Naomba mafunzo yaje kila mara ili Wabunge waelimishwe. Wakielimishwa Wabunge kazi hii itakuwa rahisi. Tulikuwa na Mheshimiwa Keissy, alikuwa champion wa kupambana kuona wafugaji wanaonewa. Nikamwambia utaingia Kamati ya Selous. Aliyoyaona, mwenyewe amekuwa mpenzi mkubwa wa wanyamapori na tukamaliza migogoro hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia suala la mjusi. Najua muda wangu ni mdogo sana. Nimelizungumzia suala la mjusi toka mwaka 2005. Hii maana yake, nami nahisi hata uchaguzi wangu nimekuja ili kuhakikisha suala la mjusi tunalimaliza. Nawe Mbunge, kama Naibu Spika ni champion naomba uwe mmojawapo katika ma-champion wa kupambana na kuhakikisha pato la mjusi linarudi katika nchi hii. Kwa maslahi mapana ya nchi yangu, nasema karibu sana. Tuko Wajumbe 20, lakini naona na wewe hutalikataa hili, unakaribishwa sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mjusi, fossils ambazo zimetoka Lindi, sasa hivi ziko sita Ujerumani. Vile vile tumeambiwa duniani kuna ndege wakubwa sita wametoka Tanzania, wako Ujerumani. Wengine wakaniambia, mama bado, ongeza harakati. Kuna vyura wa Kihansi, wako Marekani. Tunataka tujue sisi tunafaidika nini na vyura wa Kihansi ambao wako Marekani? Tumeambiwa tena kuna chameleon wako Australia. Tunataka kujua kule Australia tunapata faida gani na wale chameleon wetu wale, hawa nanii… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Chameleon kwa maana ya kinyonga au?

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, eeh, ni vinyonga. Nisamehe sana, nimesahau Kiswahili kidogo, lakini nitazidi kujitahidi. Chameleon wako Australia kule, lakini tunataka kujua tu wamefikia vipi? Bado ni maliasili, inabidi tuisimamie na tupambane nayo. Kuna vichwa vya watemi viko Ujerumani, vilichukuliwa miaka mingi sana. Tunaomba tusimamie nayo. Hivi tunachozungumza, suala la hakimiliki, hata kama walichukua wakati wa Ukoloni, lakini Tanzania it is the sovereign state na tunajua kabisa Balozi wa Ujerumani amemleta mwakilishi wake. Tunataka tukitoka hapa mwezi wa Saba tunakwenda kufanya event kubwa Tendeguru na tunataka tutengeneze MoU, Tanzania ipate tozo kutokana na mapato ya mjusi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haki ya mtu hailiki, ni lazima tupambane nayo na tukipata pato lile, nina imani kwamba nitakapoondoka hapa Bunge nitakuwa nimeacha legacy kubwa sana na kuhakikisha Wabunge wenzangu wanapotoka hapa, watakuwa champion wa kusimamia maliasili yetu ya Tanzania ambayo inatoweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia suala la NIASA Selous Corridor; ni kama la Serengeti, Masai Mara. Wanyama wanatoka Tanzania Serengeti wakielekea Kenya na imetangazwa sana, lakini hii ya Tanzania ya Selous NIASA haijatangazwa. Hii ni Mbuga rasmi ya tembo. Nataka nikuambieni tu angalizi, hii mbuga imevurugwa sana na kutoa vitalu pembeni kabisa anapopita tembo. Hivyo, ina maana tembo akipita pale anavurugwa.

Nilihudhuria katika Mkutano wa WTO wakasema Tanzania it is a lost Eden. Mmeiacha Eden nzuri ya tembo inavurugwa na matokeo yake kwa vile Wabunge hawajui wanachokizungumza, wanaona wanaonewa, kumbe wao wanawaonea wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, corridor zote za wanyamapori zimekuwa intervened. Sasa unajiuliza, tembo inabidi apite katika Miombo Forest, atapita wapi na ninyi mmeshaiharibu? Misitu mmeshakata, mmefanya fujo kubwa ya kukata misitu. Je, hawa wanyama watakwenda wapi? Simba wamemalizika mpaka hadi mwisho Serengeti unauliza, sharubu yuko wapi? Hii yote ni fujo ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mikoa ambayo hata umwambieje, yeye kila siku anataka kula kimolo. Wanajijua wenyewe! Sasa ukiona watu wale wanapenda nyamapori maana yake wao ni majangili, ni watu ambao wanafanya uharibifu mkubwa kwa wanyama. Tulikuwa na tembo kuanzia 2,000,000, wakaisha wakafika mpaka 300,000, wakafika mpaka 100,000, wakaisha mpaka 10,000. Tushukuru katika Serikali ya Awamu ya Tano tumewarudisha mpaka 47,000. Bado hatujafikia kundi la tembo tunalohitaji. Sasa kinachofanyika ni majangili wanafuata tembo. Wakiwafuata tembo, ni lazima na tembo naye atakuwa hakubali, atawaua. Sasa hapa lazima tukae chini. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru sana. Napenda wanyamapori, napenda uhifadhi na utalii. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii, nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijaalia nami kupata nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mezani, na kukiombea rehema Chama changu cha Wananchi CUF kupitia kwa Katibu Mkuu wangu Maalif Seif aendelee kuwa na subira na Mwenyezi Mungu amesema, Innallah Maa’swabiriina (kila mwenye subira yuko pamoja na Mwenyezi Mungu). (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiangalia hotuba na hoja zilizopo mezani kwangu hazihitajiki kuungwa mkono na Wabunge wa Mkoa wa Lindi na Mtwara. Nina sababu za msingi ukienda ukurasa 188, bajeti ya miradi ya Mkoa wa Lindi, ukichanganya na Mkoa wa Mtwara basi zinazidi Mkoa wa Kilimanjaro. Mkoa wa Lindi na Mtwara ukichanganya tunapata shilingi bilioni 1.7; wakati ukizingatia Mkoa wa Lindi ni Mkoa wa mwisho. Leo Mbunge wa Liwale hawezi kwenda Liwale hana nafasi barabara hakuna. Mbunge wa Liwale anatoka Dar es Salaam mpaka Lindi - Masasi - Nachingwea anakwenda Liwale na hawezi kufika kwa siku moja. Ameanzia Mheshimiwa Kawawa akashindwa, wamekuja Wabunge akina Hassan Chande Kigwalilo wameshindwa, halafu utasema tuna sera ya barabara, siikubali sera hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni sera ambayo inabagua, ni sera ambayo ina upendeleo, ni sera ambayo haitaki maendeleo ya watu wa Kusini. Wameitengeneza sera hii maksudi watendaji kuhakikisha Kusini inadhalilika. Nazungumzia hivi kwa sababu Mkoa mzima wa Lindi una miradi minne tu. Je, jiulizeni ukiangalia Jimbo la Lindi Vijijini la Mchinga na Mtama hawajaweka mradi hata mmoja, tujiulize kuna nini? Kujiuliza maana yake unapata maswali mengi ukijiuliza, eti kweli barabara za Mchinga hakuna hata mahali pa kufanya rehabilitation? Hakuna ndani ya kitabu hiki. Mtama kwenye Jimbo la mdogo wangu au mwanangu Nape Nnauye hakuna hata mradi mmoja, ninyi ni wabaguzi! Mnaibagua Kusini kwa maksudi kuwafanya wananchi wa Kusini waichukie nchi yao kwa ajili ya miradi yenu mibovu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani watu mikoa mingine wana lami mpaka katika kata, leo Mkoa wa Lindi hauna mawasiliano ya aina yoyote sasa hivi. Nakwambia utasikia wanakwenda mikoa mingine siyo Lindi, viongozi wakuu juzi wametembelea kwenda Lindi wameshindwa kwenda Liwale, wameshindwa kwenda Nachingwea, kwa nini wameshindwa? Hakuna njia ya kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ubaguzi huu ndiyo unaofanya wananchi wa kule kuichukia CCM. Na mimi naungana nao kuichukia CCM kwa vile hawataki kuwatendea haki, barabara iliyopo ni ya kitaifa ambayo ni lazima muijenge, jiulize unatoka Nanganga kwenda Nachingwea haipitiki, unatoka Nachingwea kwenda Liwale haipitiki, unatoka Liwale kwenda Nangurukuru haipitiki, unatoka Lindi - Ngongo mpaka kwenda Ruangwa hakupitiki, halafu mtasemaje sisi tuko katika Tanzania, sisi tuko Tanganyika. Ndiyo maana tunaidai Tanganyika na makao makuu ya Tanganyika yatakuwa Liwale. (Makofi/Kicheko).

Mheshimiwa Naibu Spika, kumetokea mafuriko, Jimbo linaloongoza kwa mafuriko ni Lindi Vijijini. Jiulizeni wapi wameweka bajeti ya Lindi Vijijini. Hawakuweka hata barabara moja ambayo itarekebishwa angalau wananchi wale wapate hifadhi, hakuna. Wanawake wanatembea na miguu hakuna daraja, wanawake wanataka kwenda kujifungua hospitalini hakuna daraja watapita wapi kama siyo ubaguzi mkubwa unafanyika namna hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wanaosifia wamefaidika na hili, ukimuona mtu anasifia anafaidika na hili lakini mimi nitasifia kwa lipi hapa? Hakuna cha kusifia hapa. Tunadhalilika, nitashangaa kusikia Mbunge wa kutoka Lindi anaisifia bajeti hii, hakuna kitu hapa. Huu ni udhalilishaji wa muda mrefu, mimi niko humu ndani kipindi cha tatu kila mwaka ni barabara, wakienda kutafuta kura wanawadanganya, mwaka huu kutoka Nangurukuru mpaka Liwale mpaka Nachingwea ni lami na tayari tulishatenga fungu. Tupo katika feasibility study zaidi ya miaka 40 hamna feasibility study. Ifike mahali mdanganye watoto wadogo sisi ni watu wazima sasa hivi, hata wale walioko kule ndiyo maana wamegeuka wameona kabisa maeneo ambayo yamedhalilishwa, hawapewi manufaa yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo katika mazingira haya, nani atakwenda kufanya kazi Liwale? Ndiyo maana unaambiwa Mkoa wa Lindi na Mtwara ni Mikoa ya mwisho kwa elimu. Kiwango cha elimu kimekuwa chini walimu hawataki kwenda. Sasa mnataka kutuweka mpaka lini tuwe tunadhalilika tukiwaangalia tunawabembelezeni, bajeti bajeti, sera iko wapi ya barabara?

Naomba kama kweli wale Wabunge wa Kusini wana ukereketwa tukutane Jumatatu, tufanye kikao tuikatae hii bajeti haifai kabisa. Ni bajeti ambayo haimsaidii mwananchi wa Lindi wala mwananchi wa Mtwara. Kama hutafanya vile pengine unataka Uwaziri, huwezi kupata Uwaziri katika kipindi hiki. tunachoomba tuungane, tuikatae bajeti, ili itusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la wizi katika mitandao na hasa katika kampuni ya Airtel. Wananchi wanaibiwa vibaya sana pesa hasa kipindi cha sikukuu na kipindi cha weekend. Wizi huu unafanywa na wafanyakazi na ninao ushahidi nitakuletea. Bahati mbaya walinifanyia hata mimi mwenyewe, lakini nikawaambiwa ninyi mmechezea choo cha kike na leo mtakiona. Walifanya wizi baada ya kuletewa pesa za Mbunge mwenzangu alifiwa wakanitumia pesa katika simu yangu. Wale kule wanaona kama imeingia na ilikuwa ni kipindi cha sikukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikapigiwa simu; mama kuna pesa ilikuwa zimekatwa kimakosa tuanaomba tukuingize, wakanipeleka nikashtukia sielewi maana yake ilikuwa siku mtandao haufanyi kazi, nika- qoute agent code namba nikai-qoute, ghafla nikashtukia milioni moja laki tano wameziiba.

Walipoziiba hela zile nikakimbia nikaenda Dar es Salaam nika block, kinachosikitisha watu wa cyber crime wakishirikiano na taasisi hizi hazina mawasiliano. Sasa jiulize kama watu ambao wanaweza kujitambua wakajua wafanye nini ili waweze kurudisha hela zao, je, watu wa vijijini wanafanya nini, ni kuibiwa tu. Wizi umekuwa mkubwa sana tunataka tupate majibu hawa watu wa cyber crime wanafanya nini, mbona wizi umekuwa mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano ukienda India unaambiwa utakaa kwa siku ngapi ukipewa ile card chip ya kukaa pale, unasema nakaa wiki mbili, siku unaondoka ikifika saa sita usiku jina lako limeshapotea na mawasiliano yamepotea. Tanzania acha simu yako nenda kakae Marekani miaka miwili ukirudi unakuta matandao uko online tu, mpaka leo hawajahakiki kama kweli jina lile linalotoka katika namba ndiyo kweli, wenzetu Uganda wameshaanza sasa hivi kuhakikisha yule aliyepewa namba kweli ni mwenyewe, ndiyo maana wizi wa mtandao hautaweza kuisha kutokana na uhakiki wa majina haukufanyika vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Wizara yenye dhamana ifanye kazi ya kuhakiki vizuri.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niipongeze Serikali naipongeza Serikali kwa kupitia mtandao wa mwendokasi wameshinda tuzo kwa kwa kuweweza kufanya uwekezaji mzuri katika Afrika Tanzania ni nchi ya pili.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RIZIKI S. LULINDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nami kwa kunipatia hii nafasi ya kuchangia hoja ya Wizara ya Maliasili. Mimi naitwa Mama mjusi, Mama Selous, Mama Mazingira lakini vilke vile ni Balozi wa Utalii; nilipewa tuzo hii na Mheshimiwa Rais. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa tuzo aliyonipa, kwa hiyo nitasema nitaongea ukweli na sitamwangusha. Kwa vile mimi ni mwanahifadhi lazima kwanza nitasimama na hifadhi na haki za binadamu ndani ya maliasili zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, nilikuwa naye katika michezo, kazi aliyoifanya katika michezo mpaka timu ya watu wenye ulemavu tuliweza kufikia katika mpira wa World Cup. Na imani yangu wale waliokwenda kurithi kule watafanya kazi kama aliyofanya Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu tufike tena, maana mwaka huu tena kuna mpira wa Afrika utafanyika Misri. Matumaini yangu ni kwamba timu yangu imejiandaa, na wale tuliokuwa naowalioingia sasa hivi tuwe nao vizuri ili hawa vijana ambao wamecheza katika mpira wa watu wenye ulemavu; sasa hivi tunazungumzia vijana kumi wako Ulaya huko wanalipwa katika professional soccer; Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu hongereni sana. Vilevile nimpongeze Naibu Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya ya kupambana na hali ngumu sana. Hii ni Wizara moja wpo katika Wizara ambazo ni ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi katika uhifadhi nitazungumzia kwanza Mbuga kubwa, ikiwemo Ruaha, Serengeti lakini pia tuna Mbuga ya Selous nayo ni mbuga kubwa ya kwanza Afrika lakini ya pili duniani. Lakini niizungumzie ya tatu, tuna corrido za wanyama ambazo ni ambazo wanapita. Asilimia 20 ya ardhi ya Tanzania ilitengwa kwa ajili ya uhifdhi, faida yake ya Uhifadhi tumetegemea kupata mvua, tunategemea mito itatiririka ili maji yasaidie katika kilimo, hivyo kuondoa uhifadhi ndio maana unaona sasa hivi ni ukame unakuwa mwingi kutokana na maeneo mengi yameharibiwa. Mimi nalizungumza hili kwa ninayoyajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbuga ya kwanza ambayo ninataka niizungumzie ni Mbuga ya Ruaha (Ruaha National Park). Ruaha National Park inategemea maporomoko ya Congo Basin ambayo yanateremsha Usangu, Usangu inaingia Ruaha, Ruaha maji yake yanakwenda Kihansi, kilombero yanaingia Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya maji yanasaidia Wizara ya Nishati na Madini, tukiyaharibu maeneo haya nchi itaingia gizani na matokeo yake itakuwa ni malalamiko makubwa zaidi. Na gizani hapa siyo Tanzania Bara tu, umeme unatoka katika maeneo ya Kilombero mpaka Rufiji unakwenda mpaka Zanzibar. Ina maana nchi itakuwa gizani, na itakapokuwa nchi gizani uchumi wa nchi utaporomoka, hivyo tuwe waangalifu sana. Na ukiangalia Ruaha National Park ukubwa wake si mkubwa hivyo kama watu wanavyofikiria. Niliangalia katika google wameniambia Ruaha National Park ina ukubwa wa square mita za mraba 13,800, nimeangalia Selous 44 niliangalia Serengeti 12,500. Niwapongeze ma-DG, Wakurugenzi Wakuu wa TANAPA, Mkurugenzi Mkuu wa Ngorongoro, TAWA na washikadau wote wa maliasili kwa kweli wanafanya kazi kubwa sana ya kupambana na watu ambao si waaminifu. Kuna watu waaminifu na watu wengine wanaingia ndani siyo watu waaminifu. Mimi nuilikuwa na mojawapo mdau ambaye nimezunguka Tanzania nzima na Wabunge baada ya kupata kelele kelele hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge tukaenda kujionea uhalisia, wafugaji wanaingia ndani ya mbuga na ng’ombe wakiwa na bunduki za kihalifu machine gun. Hivi kweli wewe katika mbuga kuna simba kuna tembo, kuna nyati makundi kwa makundi, wewe unaingiaje pale, ina maana wewe ni muhalifu na wafugaji wengi wanatumika. Tukubaliane Waheshimiwa Wabunge wafugaji wengi wanatumika na una muona mfugaji ana mifugo 4,000, ukiwa na ng’ombe 4,000 zungumza kuwa wewe ni bilionea una bilioni 1.2. Kitu ambacho hata Mbunge sitegemei kuwa na hela kama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yangu tufanye database ya kuwajua wafugaji wote wenye ng’ombe wengi halafu tuwatengenezee mifumo utajiri wao ule uweze kuwasaidia na tutajua kama wafugaji hawa ng’ombe wale ni wao au wanatumika na watu wengine kama mlivyoona Ngorongoro. Katika kuhamisha Ngorongoro tulitegemea watu watakuja Handeni na ng’ombe wengi sana. Waliambiwa kuna ng’ombe 5,000, 4,000, 3,000 siku wanakuja kuhama mtu anakuja na ng’ombe watano, ng’ombe 10 kitu ambacho mengi yalioletwa katika taarifa unaweza ukapata katika mitandao ni vitu vya kuzusha na kuwafanya watu na nchi iingie katika taharuki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumza hiyo ukiichukulia Mbuga ya Serengeti kwa ukubwa wa square mita za mraba 12,500, kwa kweli unategemea Mto Mara upate maji na kama utakuwa unategemea Mto Mara kupata maji watavua, watapata samaki na vitu vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unamuona mfugaji anaingia mule ndani kila siku tumege tumege tukapomaliza kumega mtasema bado Mto Mara umeshakauka. Je, mimi nayaona mapori makubwa makubwa yameachwa Tanzania hayajatumika, naomba Wizara ya Ardhi isimame na Wizara ya Maliasili watengeneze mfumo na mpango mkakati wa kuhakikisha baadhi ya wafugaji wanakaa katika mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano hai, wafugaji walipelekwa Mkoa wa Lindi, Mtwara walikataa leo Lindi maeneo yote waliyopewa wamehama, wamekimbilia Selous, unaona neno hilo. Wamehakikisha kuwa misitu yote kuanzia Rufiji wamekata na sasa hivi Lindi ni jangwa. Wamekimbia maeneo walipewa kila mfugaji square mita za mraba 5,000 mtu wa kawaida ambaye huwezi kupata lakini wameshakata misitu, wamekata kila kitu wamechoma mkaa, sasa hivi tunazungumzia Selous wanakwenda Selous. Sasa tunajiuliza kweli huu ni ufugaji au ni uharibu, tujiulize na tujipe tathmini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbuga ya Tendaguru; Tendaguru ni eneo ambalo tuna misitu ya na miti aina ya mipingo hapa ndipo alipotoka yule mjusi mpaka mimi napata jina la Mama mjusi. Tumekwenda na Naibu Waziri, wafugaji wote wamehamia pale waliokatiwa maeneo yao maeneo chungu nzima walipewa wamekwenda kukaa Tendaguru. Matokeo yake Tendaguru tembo hawakanyagi anamuogopa mfugaji, Tendaguru simba hakanyagi anamuogopa mfugaji, Tendaguru unaiona imekaa pale wamejaa wafugaji na mifugo yao wanaharibu mazingira wanamaliza miti ya mipingo kauli za viongozi nazo zinarudi kwenda kuangali nilitoa amri hawa wafugaji waende katika maeneo yao lakini bado wamebakia maeneo hayo kwa nini hawajaondoka lakini akiongea mtu akiondoka wafugaji hawagusi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo tunaizungumzia Milola, tembo wanakimbilia Milola tembo wanakimbilia maeneo ya pembeni kwa vile nini, maeneo yao yamezingirwa. Tunaanzia Nyasa anavukwa corridor kuingia Namtumbo, corridor limevamiwa na hizo ziko ndani ya GN. Tunatoka Namtumbo tunaingia ndani ya Selous wafugaji wako ndani ya Selous hivyo wakikaa ndani ya Selous na wanaingia na magobore tembo wanakimbia katika maeneo ya wakulima.

Mheshimiwa Spika, sasa hii kitu tukubaliane ninaomba tukitoka hapa tutaandaa timu ya kuhakikisha timu hii itakwenda kujua wafugaji hawa ni wapi? Na ni wachache kweli, wafugaji wako Kilimanjaro, wanafuga hakuna migogoro, wafugaji wako Arusha, wanafuga hakuna migogro wafugaji wako Shinyanga Mwanza lakini hawa wanayehamahama si wafugaji ni wafanyabiashara na wanatumika na hii kutumika tunaifanya nchi ina - paralyze. (Makofi)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lulida pokea taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa Mama yangu pale Mheshimiwa Lulida, kwa kweli kule kusini hakuna wafugaji kule kuna wachungaji. Wafugaji wapo hapo Ruvu kama ulivyosema wako Ruvu wako huko Kigoma wapo hapo Kongwa wale ndio wafugaji, kule kuna wachungaji na ndio maana wanasumbua.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Riziki Said Lulida, unapokea taarifa?

MHE. RIZIKI SAID LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapokea taarifa mimi natoka Selous, nimezaliwa Selous, ninaijua Selous tumekaa na tembo tukiwa marafiki lakini baada ya …

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, … wafugaji kwenda kuhama hama Tanzania nzima leo nasikia Mbeya…

MWENYEKITI: Ahsante sana na muda wako umekwisha.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haijafika dakika kumi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia kuwa na afya njema na kuniwezesha kuchangia katika hoja iliyopo Mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara ya kwanza nataka niishukuru na kuipongeza timu ambayo ilisimamia kuhakikisha Tanzania concession fee inapita na kuifanya Serikali iweze kupata mapato. Nitataja kwa majina ni akina nani walisimamia hiyo timu, ilikuwa chini ya Mwenyekiti wa Bodi iliyopita Ndugu Modestus Lilungulu, Mama Chijoriga, Ndugu Fumbuka, Mama Wilmo, Mheshimiwa Jenista Mhagama na mimi mwenyewe Riziki Lulida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtajiuliza kwa nini tumefikia hapo? Tanzania tulifikia mahali ambapo uchumi wetu ulikuwa nyuma, watu walikuwa hawataki kulipa tozo ambayo ni halali katika nchi hii. Tozo ya dola nane katika hoteli ni hasara kubwa katika nchi hii na uchumi mkubwa unakwenda kwa wawekezaji sisi wenyewe Watanzania tunakosa mapato. Nilimwomba Waziri Mkuu ashirikiane na Wizara watufanyie semina, namshukuru juzi tumepata semina ya kwanza, bado haijatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haijatosha kwa vile watu wengi au baadhi ya Wabunge bado hawana uelewa. Ili kujenga uelewa kwa Wabunge wapya, kwanza watembezwe katika maeneo husika wajionee kiasilia. Leo unaona mwenye hoteli anatoza dola 500 anataka atoe dola nane lakini jiulize TANAPA ndiyo wanajenga barabara, wanapeleka maji, TANAPA na Ngorongoro ndiyo wao wanapeleka maaskari kutunza maeneo yale ili watalii wawe katika usalama. Je, mnaposimamia tozo hizi ziendelee kuwa kwao sisi wenyewe tuendelee kupata tabu, ni nini hicho? Maana yake hatujafunguka. Ili tufunguke, naomba tena tuje tufanyiwe semina mbalimbali ili watu wapate uelewa (awareness creation) kwa ajili ya Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha mwekezaji anaingia ndani ya mbuga, ana hoteli lakini anaingiwa na kigugumizi cha kutotaka kulipa kodi na anatumia mbinu zote mpaka kwenda mahakamani toka mwaka 2007 na ndiyo sasa hivi concession fee imeruhusiwa na tutalipa katika fixed rate ambapo uchumi wa nchi utaruka. Baadhi ya Wabunge mnasema tusilete hizi tozo, kwa faida ya nani? Tuna ajira ndani ya TANAPA, watoto wetu, ndugu zetu wanafanya kazi watapata wapi mishahara? Kuna tour operators ambao wanakuja kufanya kazi Tanzania na wana wafanyakazi, kama tozo hizi mnataka zirudi kwa upande wa pili hela hii itapatikana wapi? Ndiyo maana nasema tupewe semina tena ili kujenga uelewa wa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nizungumzie Mbuga kubwa ya Selous. Selous ni mbuga ya kwanza kwa ukubwa Afrika, lakini ni mbuga kubwa duniani lakini hakuna chochote kinachofanyika ndani ya Selous hata mapato hayaonekani. Kuna corridor ambayo inatoka Mozambique inakuja Tanzania, kila mwaka tembo, simba, chui na nyati wanakuja Tanzania, haijatangazwa hata siku moja, kila mwaka inatangazwa Mbuga ya Serengeti. Kwa nini mnaiacha Selous isitangazwe halafu mnaridhia kuwapa percent ndogo ya 17.2. Jamani tufike mahali tufunguke tuinue uchumi huu kwa kuiongezea pesa za promotion ili Selous ifanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Selous na ukubwa wake lakini two third ya Selous ipo Mkoa wa Lindi na Mwenyezi Mungu ameujalia Mkoa wa Lindi kuna fukwe kubwa za bahari kuanzia Lindi mpaka Mtwara. Kwa nini Selous isingefunguka ili ikasaidia uchumi wa kusini, Selous imefungwa. Ni uwindaji na ujangili kwa kwenda mbele matokeo yake tunapigania uchumi ambao umefungwa na baadhi, sielewi kama ni makusudi au ni dhamira. Nataka kesho Waziri atakapokuja kufunga hoja yake aniambie kwa nini Selous haiwi utilized. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwenda Liwale kwenye Selous yenyewe hakuna barabara, kutoka Nangurukuru kwenda Liwale mpaka Nachingwea ambayo Selous inachukua asilimia 2.3, hakuna barabara. Nataka Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano akishirikiana na Waziri wa Maliasili na Utalii watujibu kwa nini wameifunga Mbuga ya Selous isifanye kazi? Imefikia mahali tunajiuliza, tunataka uchumi endelevu na uchumi upo na wanakuja wageni wakileta fedha za kigeni lakini unaona ajabu Selous haitumiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia uchumi wa utalii ambao uko ndani ya Tanzania na ukitaja Tanzania ni lazima na Zanzibar uitaje. Utalii huu Bara unaonekana lakini Zanzibar haionekani. Ili kuondoa umaskini ni lazima kuhakikisha maeneo yote haya mawili yanaendelezwa kiutalii. Maana yake mtalii anatoka Ulaya akiwa na package kuwa anaingia Serengeti, Ngorongoro anamalizia Zanzibar, kwa nini Zanzibar pesa hakuna, kwa nini Zanzibar wasifunguke na utalii huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo madogo kama Seychelles, ni nchi ndogo lakini utalii na uchumi wao ni mkubwa lakini Zanzibar imedorora. Lazima tujiulize kuna nini Zanzibar mpaka utalii wake uko mikononi mwa wajanja na Wazanzibari wenyewe inabidi wafunguke. Humu ndani kuna Wazanzibari, tumieni fursa yenu kuiona Zanzibar inakwamuka na utalii wa Zanzibar unafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mwenyekiti wa Kupambana na Ujangili ndani ya Bunge, nataka kuzizungumzia corridors. Corridors kubwa za tembo Tanzania moja ipo Rukwa (Rukwati) na nyingine ipo Niassa (Mozambique). Corridor ya Rukwa (Rukwati) ambayo inatokea Zambia inakuja mpaka Katavi haitangazwi, vilevile ya kutoka Mozambique kuja mpaka Tanzania haitangazwi matokeo yake wameingia wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikupe taarifa, nikiwa na mwenzangu Mheshimiwa Jenista Mhagama, tulikutana na kundi la ng’ombe, wale wafugaji wakiwa na silaha wanaingia ndani ya mbuga. Tukajiuliza wanakwenda kufanya nini ndani ya mbuga, kuna tembo, simba, faru na nyati, kuna harufu kubwa ya baadhi ya wafugaji kushirikiana na majangili. Hivyo, Wabunge mtapendelea ufugaji lakini mnashindwa kuelewa kuwa hao wafugaji sio wote ni wafugaji wengine wanatumika. Hivyo, elimu ya wafugaji itolewe na wenyewe wafunguliwe kuwa wengine wanatumika ndiyo maana unaona ujangili unaingia ndani ya mbuga kwa kupitia hao wafugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sina mengi sana, nawashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia sisi wote kuwa na afya njema kuwepo hapa. Mimi ni balozi wa utalii, lakini mimi ni Mwenyekiti wa Caucus ya Bunge ya kusimamia ulinzi wa wanyamapori akiwemo tembo na wanyama wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile mimi ni mama mjusi, nalizungumzia suala la mjusi kwa miaka, lakini leo nitazungumzia sana suala la Selous. Nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa sana aliyoifanya ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni kote kwa kupitia Royal Tour na nilizungumza miaka nyuma Tanzania inahitaji kutangazwa na utangazaji wake wa namna hii, tunahitaji kutangaza katika mitandao mbalimbali ikiwemo hii aliyoifanya kwenda Marekani kuitangaza Royal Tour na kwa kweli dunia kwa ujumla wake umemtambua kama Tanzania ina vivutio vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania ina vivutio vingi na hasa ukiangalia katika kanda, kuna kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kule tunakwenda Katavi kuna Rukwa Lukwati hili ni eneo la wanyamapori ambao wanatokea Zambia kila mwaka wakija Tanzania wakifika mpaka katika mbuga za Katavi na kuendelea sehemu mbalimbali iwe Gombe na baadhi ya game reserve. Ni hasa Selous corridor hii corridor ni maalum Mwenyezi Mungu aliiumba ile corridor na corridor ile ni kwa ajili ya tembo, nyati, simba, mbwamwitu wale wanatoka katika hifadhi ya Nyasa wanavuka Mto Ruvuma kwa makundi kama ile ile kwa Serengeti Masai Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Watanzania tukubali tunahitaji uchumi, tunahitaji maendeleo, lakini tunahitaji wananchi wetu. Hawa wananchi wengine wasijiingize katika migogoro ya wanyamapori, mimi mwaka 2014 nilipewa nafasi ya kuzunguka na Wabunge na ndio maana nasema elimu kwa Wabunge inabidi iletwe hapa ndani watambue haki za wanyamapori na haki za binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili kuondoa migogoro ambayo inaitwa wildlife and human being conflict, tukifanya hivyo wanadamu wataacha kuziharibu njia za wanyamapori, ukitoka Nyasa unataka kuingia Namtumbo, binadamu wame- intervein njia za tembo, tembo anashindwa pakupita anaingia katika mashamba ya watu, hivyo anashindwa kuingia Selous mle ndani ya Selous binadamu amejiigiza mle ndani anafanya uwindaji haramu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi mwenyewe nilipewa fund na GIZ kuzunguka na waandishi wa habari, tumevumbua mambo mengi sana ya binadamu. Nilikuwa na mama Mary Masanja tukaenda Tendaguru wamevamia wafugaji wako ndani ya Tendaguru wanyama wote wanakimbia na wanapokimbia hawana mahali pa kwenda wanakwenda kwa binadamu. Nafikiri Mama Masanja ni shahidi, sasa akatoa tamko kuwa atakapokwenda tena wale watu watakuwa wameoondoka wote na alitoa taarifa kwa Mkuu wa Wilaya wavamizi wote waliovamia katika eneo la Tendaguru waondolee nataka nipate majibu akitoka hapa je maagizo yale yametekelezeka?

Mheshimiwa Spika, leo unamkuta tembo anataka kutulia Tendaguru tena msitu mkubwa sana, lakini binadamu mle amekaa analima katika hifadhi ambayo imeshatunzwa iko chini ya TFS sasa unasema migogoro mingine ni binadamu anasababisha migogoro hiyo kwa ajili ya kupitia njia ya wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaizungumzia Selous ambayo ni mbuga ya kwanza katika Afrika, lakini ni mbunga ya pili duniani kwa ukubwa, na Selous inazunguka katika mikoa sita Mkoa wa kwanza naanza Morogoro, Iringa, Ruvuma, Pwani Lindi na Mtwara katika hiyo mbunga ndio inazunguka humo ndani kuna wanyama wa kutisha, lakini sasa nenda ndani ya Selous utaona ni vurugu tupu binadamu anavamia anachimba humo ndani, lakini maendeleo yote hayapelekwi Selous, maendeleo yanapelekwa Kaskazini tu.

Mheshimiwa Spika, sasa tujiulize kama huko hamkuangalii mtategemea migogoro haitakwisha? Nimesikiliza katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri humu ndani kote wamepanga fund lakini siioni fund ambayo itakweda Selous haipo, lakini jiulize kama mbuga kubwa kama hii inaachwa tunategemea kuna maendeleo makubwa ya kimkakati? Mikoa hii kwa mfano Mkoa wa Lindi, Ruvuma na Mtwara tuna mradi mkubwa wa LNG unakwenda katika miaka mitano kama mkipanga watalii na watu mbalimbali watakaotembelea Selous tulitegemea.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, tulitegemea itakuwa na miundombinu, lakini kama hamjatengeza miundombinu msitegemee mafanikio katika Selous.

SPIKA: Mheshimiwa Riziki Lulida kutoka kwa Mheshimiwa Zuberi Kuchauka.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi, nataka nimpe taarifa mama yangu anayechangia, kuna fedha zilitoka kwa ajili...

SPIKA: Ngoja, ngoja anaitwa Mheshimiwa Riziki Lulida.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, sawa Mama Lulida.

SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, nilitaka nimuongozee taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka, anaitwa Mheshimiwa Riziki Lulida.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Riziki Lulida. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nilitaka nimpe taarifa mchangiaji kwamba anavyosema ni sahihi kabisa kwamba kuna fedha zilitoka kwa ajili ya utalii Kusini zile fedha ziliishia Mikumi. Kwa hiyo kwa mujibu wa taarifa za Wizara ya Maliasili wao Kusini maana yao ni Mikumi na Iringa sio Lindi na Mtwara. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hizi taarifa hizi tunazozisema humu ndani hizi tuwe makini kidogo. Mheshimiwa Riziki Lulida.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, taarifa naipokea hizo fedha zilitolewa na World Bank kwa ajili ya maendeleo ya kutengeneza barabara katika maeneo mbalimbali katika mbuga zetu, lakini nililizungumza mwaka juzi kuwa Lindi na Mtwara hela zile hazikupelekwa hasa kwa Selous na hii naizungumzia kwa vile Jimbo la Liwale ndio tunategemea kupata barabara na kuna viwanja vya ndege, lakini hazikupangiwa bajeti hata kidogo katika maeneo hayo. Hivyo matokeo yake mtalii anavyotaka kwenda kuwinda Liwale inamuia vigumu sana kwa vile hakuna njia ya kupita kumfikisha Liwale na wala barabara ya kutoka Dar es Salaam au kutoka Nangulukuru kwenda Liwale inapitika kwa msimu, hivyo taarifa yake naipokea.

Mheshimiwa Spika, tunataka kuisaidia Serikali katika kuendeleza utalii ni lazima tuunganishe na private sector na hii itatusaidia katika maendeleo. Nataka nitoe mfano wa private sector ilivyosaidia sekta ya utalii, Bakhresa Group of Companies ameleta meli ambazo zinakwenda Zanzibar, amefungua mahoteli makubwa Zanzibar, matokeo yake ameliletea urahisi Zanzibar kwa ajili ya watalii kwa vile watapata mahali pa kukaa, usafiri wa uhakikia kwa kutumia boti mbalimbali za Zanzibar, tulitamani sisi mkishirikisha private sector katika masulala ya maendeleo ya utalii nina imani Visiwa vya Mafia nao wataibuka katika utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona mapato ya utalii yameingia kwa asilimia tano tu, lakini kama mtafungua maeneo mbalimbali kwa mfano Kanda ya Ziwa, mkaifungulia mawasiliano makubwa kati ya Burundi, Rwanda na maeneo ya Burigi tutapata utalii mkubwa mpaka Kigoma. Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Zambia - Tanzania mkifanya mashirikiano katika masuala ya utalii tutavuta katika masuala ya utalii. Lakini Mozambique - Tanzania tukiisimamia katika hilo suala tutafika mbali katika suala la maendeleo, lakini je, tuna mahoteli? Mahoteli maana yake leo tukitangaza tunategemea tupate na mahoteli ya kuwapokea wageni wetu, tunahitaji mawasiliano ya barabara na miundombinu, leo tunahitaji fund kubwa ili hii sekta iweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwashukuru watu wa TANAPA wanafanya kazi kubwa sana, siyo kazi ndogo kushindana na binadamu, binadamu anataka kumuwinda tembo ili amuue na tembo na yeye vilevile ni mnyama mwenye akili kuliko binadamu anakuwa hakubali vilevile kuuana. Hivyo hapa ni lazima tuungane nao watu wa TANAPA, watu wa Ngorongoro na watu wa TAWA hii kazi ni kubwa binadamu anategemea kufanya ujangili apate maslahi yake. Nina mfano hai sasa hivi ujangili umerudi tena, sasa tuseme vizuri kuwa hapa ni binadamu na wanyama wako katika mgongano. Serikali simamieni tunahitaji mapato makubwa na wananchi wapate faraja kwa kupitia sekta ya utalii. Tanzania tunategemea utalii kwa ajili ya wanyama watano; simba, tembo, nyati, chui na faru. Ivory Coast walikuwa na wanyama kama Tanzania kwa fujo za binadamu sasa hivi ni historia.

Naiomba Serikali yangu na wananchi kwa pamoja tushirikiane katika ulinzi huu, siyo ulinzi wa kuiachia peke yake Maliasili, ni jambo letu na maendeleo yetu, Mama anatangaza utalii na sisi tuwe wadau wa kusimamia utalii huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nasema ahsanteni sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii na nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, aliyenijaalia kupata afya njema na kuwepo katika kuchangia hoja iliyokuwepo mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mtanzania na napenda maendeleo ya Tanzania na napenda Watanzania iwe mweusi, iwe mweupe, mwenye rangi ya kijani, tuwe na maendeleo ambayo yanawiana. Nataka nitoe pongezi zangu za dhati kwa baadhi ya wawekezaji wa Kitanzania ambao wameonesha kuwa wana uwezo wa kuweza kufanya biashara na wana uwezo kuingia katika uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 20 Mwezi Aprili, kulifanyika mkutano mkubwa sana Nairobi wa African Urban Transport. Nataka kuwapeni taarifa Wabunge mwendo kasi UDAT imepata tuzo namba mbili. Yule ni Mtanzania kama ana mahali amekosea basi inabidi arekebishwe lakini ameonesha uwezo mkubwa na wameambiwa Wakenya, Waganda, Wazambia, Waethiopia na tumewaona wamekuja kujifunza Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ndiyo maendeleo ambayo unayaona yakiwekezwa kwa ngozi nyeusi na Watanzania basi maendeleo haya yatakuwa yana uwiano, na pesa yetu badala ya kuipeleka nje, itabakia Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpongeze tena Reginald Abraham Mengi na yeye ameonesha uwekezaji wake unamsaidia na unamgusa mtu mwenye ngozi nyeusi na ajira kubwa zinakwenda kwa watu wenye ngozi nyeusi. Nampongeza Bakhresa, kazi yote na fedha zinazopatikana za Bakhresa zinabakia Tanzania na unaona hata nyumba zao na investment zao zinawagusa Watanzania na wengineo. Hii maana yake Nigeria waliwatengeneza watu weusi 150 mmojawapo akiwa Dangote ambaye anakuja kuwekeza Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaingia katika ulimwengu wa viwanda, tumewaandaa vipi Watanzania wenye ngozi nyeusi ambao ndio maskini zaidi ili waweze kuingia katika uwekezaji? Ni matumaini yangu, tusijibeze sisi wenyewe tunaweza. Mwanzo hatukuwa na elimu lakini sasa hivi tumepata elimu, watoto wetu hawa baadaye ndio wataokuwa akina Dangote wa Tanzania. Tusiwakatishe tamaa tuwape nguvu ili wazidi kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi, Mtwara na Ruvuma tumeonesha mabadiliko makubwa sana. Mwaka jana nilimuuliza swali la papo kwa papo Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusu tozo na kero ya korosho. Katika usimamizi bora unaofanyika tumepata korosho kilo moja kwa Sh.3,800, ilikuwa ni dhahabu ya kijani imewezesha kuiingizia Tanzania dola za Kimarekani 346,000,000 katika mnada wa kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pesa hizi ukizigawanya au ukazipigia hesabu kwa Tshs tumefanya mafanikio makubwa sana. Tumedhulumiwa kwa muda mrefu na wafanyabiashara wa mazao. Ningeomba speed hii iliyokwenda kwenye korosho iende kwenye kahawa, tumbaku, ufuta, mbaazi na alizeti ili Watanzania hawa ambao ni maskini waweze kufarijika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la korosho linastawi Pwani yote mpaka Zanzibar. Tuko kwenye Muungano, tusiiache Zanzibar nyuma katika kuondoa umaskini tukawa sisi peke yetu tunaendelea. Hii korosho inapatikana Madagascar, Comoro na Seychelles. Nilitegemea kwa upendo wetu tuliokuwa nao katika Muungano basi na korosho ipelekwe na kuhamasishwa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, korosho yetu imeingia dosari kubwa kwa wafanyabiashara ambao wana mazoea. Baada ya kuona tumepata soko la Vietnam wafanyabiashara wakubwa wa mazao wamezuia makontena wanaya-hold ili yule anayenunua korosho asizipeleke tena nje, hii ni dhuluma kwa Watanzania. Wamekuwa matajiri kwa kupitia Tanzania, leo wao wanakuwa matajiri hawataki waone uchumi wa Tanzania unaruka kwenda mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Waziri mwenye dhamana aliangalie hili na awaangalie wanaofanya mchezo huu, uishe. Hili ni tambazi, maana kama ni jipu limevilia limekuwa ni tambazi, nataka tuhame kutoka katika majipu tuyapasue matambazi ambayo yamezoea kutukamua na kutunyonya nchi hii ili tusiweze kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda ambavyo vilibinafsishwa nataka aniambie Mheshimiwa Waziri, je, hivi viwanda vimebinafsishwa au vimeuzwa? Kama vimeuzwa nani amenunua na kama amenunua mbona havifanyi kazi zaidi ya miaka 20?

Mheshimiwa Naibu Spika, amezungumza ndugu yangu Mwambe, huyu Mwambe ana uchungu na korosho. Kiwanda cha Lindi kimefungwa, Kiwanda cha Mtwara kimefungwa, Kiwanda cha Masasi kimefungwa, Kiwanda cha Newala kimefungwa, Kiwanda cha Kibaha kimefungwa, wao wanachukua zile korosho wanakwenda kupeleka ajira kwao, kwa nini? Hamwoni kama Mkoa wa Lindi hakuna kiwanda hata kimoja? Tutapataje utajiri katika hali ngumu ya kimaskini kama hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefikia mahali tunajiuliza hivi Lindi kweli mkoa wenye majimbo nane hatuna kiwanda hata kimoja. Kama Waziri ananibishia, aniambie Lindi kuna kiwanda fulani, hakuna, vyote havifanyi kazi, ina maana tunatengeneza umaskini Mkoa wa Lindi na Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mjumbe katika Kamati ya Uwekezaji. Nimeangalia katika makosa ambayo tumeyafanya nchi hii ni kwamba hatuna sera. Kama hatuna sera tumeingiaje katika uwekezaji wa viwanda? Tunakwendaje na maendeleo ya viwanda wakati hakuna sera? Sera ni usukani, utatoa sheria, taratibu na kanuni, hatuna. Sasa hivyo viwanda 200 vinavyokuja sheria gani itasimamia? Utaratibu gani utasimamia? Kanuni gani itasimamia? Tutarudi kule kule. Hivyo naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuleta majibu aniambie kwa nini sera ya viwanda haijakamilika mpaka leo. Tunakwenda katika ulimwengu wa viwanda, tunaendaje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikwenda mpaka kwenye madini. Tulienda katika Idara na Maendeleo ya Madini bila kuwa na sera. Tulitembelea Buzwagi hakukuwepo na sera, wamechimba mahandaki, watu wengine wameshamaliza kuchimba madini, tumeachiwa malaria katika Mikoa ya Geita, Simiyu na Mara. Ndicho tunachokataa hiki, tunataka sera ije iweze kuwakamatia wale ambapo katika upande wa environmental impact assessment.

Mheshimiwa Naibu Spika, ifikie mahali tujiulize tumelogwa na nani? Wanatuambia wenyewe, nilikaa na mtu mmoja akaniambia Tanzania is a sleeping giant na tunajitambua kabisa kama tuko sleeping giant. Kama tungekuwa si sleeping giant tungekuwa na sera sasa hivi, lakini mpaka leo tunakimbizana na viwanda lakini hakuna sera. Leo unaposema mimi mtaalam unakuja kunielimisha nini wakati huniambii nitafanya nini? Nenda TPDC, walikuja kwenye Kamati wakiwa hawana sera, strategic plan, wala action plan, kutakuwa na commitment hapo?

T A A R I F A . . .

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa ya Mheshimiwa Ally Saleh, namwambia kitu kimoja, bahati nzuri nilikwenda Lima Peru, nimetembelea mpaka Mexico walifanya makosa haya sasa hivi zile nchi ziko polluted kwa vile hawaku-update hizi sera zao, wakajiingiza katika mikataba na sheria mbovu na kuiweka nchi katika umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia madini. Leo tunaletewa na STAMICO kuwa kuna baadhi ya mashirika ambayo yameingia ubia na madini, kwa vile hakuna sera, amefanya feasibility study na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru, sina lingine. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru nami kwa kupata nafasi hii. Niungane na Mheshimiwa Ally Saleh kuhusu investment confidence haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilikuwa katika mkutano wa malaria ambao uliandaliwa na USAID na wao wameingia katika uwekezaji katika malaria, ambacho ni kiwanda kimojawapo nataka nikitolee mfano cha A to Z. Kile kiwanda kina wafanyakazi 8,000 kinalipa kodi bilioni 17, kinalipia TANESCO bilioni moja, lakini cha kusikitisha kwa vile hakuna health policy, narudia tena hakuna health policy inayomfanya yule mwekezaji awe na confidence na uwekezaji wake. Kwa mfano, yeye ana kiwanda cha kutengeneza chandarua ambazo zina dawa na zimehakikiwa kimataifa na ndani, lakini leo wanaingiza vyandarua feki kutoka nchi za nje ambazo yule mfanyabiashara analipa kodi, yule anaambiwa kwa vile chandarua tunagawa bure anaingiza bidhaa zile bure. Tunajiuliza, tuko tayari kusimamia viwanda vyetu au bado tunakutana na kipingamizi kikubwa kwa vile hatuna sera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza hapa kuwa nchi hii bado hatujaingia katika sera ya viwanda na tunakwenda katika viwanda, sera iko wapi? Matokeo yake huyu anaingiza hiki, huyu anaingiza hiki, matokeo yake kiwanda kitakufa, watu 8,000 Watanzania waliopata ajira, zitakuwa zimepotea. Ushuru mkubwa anayepeleka tax ya bilioni 18, huyu anaingiza bidhaa kutoka nje, even price control inakuwa haipo. Tunataka tufanye kazi tukijua tuna idadi ya kiasi gani? Quantity, quality, price na time delivery inatakiwa ijulikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama tunakwenda katika uwekezaji wa kiholela bado viwanda vyetu vitakuwa vinasuasua, wanaleta wawekezaji wa nje, ndani watafunga hivi viwanda na tutakuwa hatuna kodi, wala kutakuwa hakuna ajira. Tuwe wa kweli, tusimamie sera, wailete Bungeni
tuifanyie kazi, lakini wakiendelea viwanda, wakati hakuna sera, kutakuwa hakuna biashara wala hakuna maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mdau natoka Lindi, Selous ni mbuga kubwa naizungumzia huu ni zaidi ya mwaka wa kumi, lakini jiulize kama TANAPA, Serengeti ni ndogo inaingiza bilioni 100, Selous hamna kitu ni ubabaishaji, kuna nini hapa? Kwa nini kuna kigugumizi ndani ya Selous? Korido ya Seleous ambayo ina tembo inafanyiwa promotion gani? Hakuna. Wanakwenda kuwakamata akinamama wauza maandazi, wanaouza mitumba mikononi, lakini wanaacha mabilioni ambayo yako katika Selous. Ili nchi hii iendelee tunahitaji uongozi, siasa safi na watu. Sasa kama vitu hivi havisimamiwi kwa pamoja itakuwa hatufanyi kazi ambayo imetuleta hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena kuhusu suala la mjusi. Mjusi ukiingia ndani ya exhibition unalipa Euro 24 kwa mtu mzima, kwa watoto wanaingiza kwa Euro 12, lakini kwa mwaka wanaingiza Euro milioni 600. Uki-convert into Tanzanian shillings unapata trilions of trilions. Sisi tunapata nini? Jamani hata tukitaka revenue au kukaa chini tukatengeneza mrabaha, nchi ikajipatia hata angalau bilioni 200 haiwezekani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafumba macho wanaangalia vitu vidogovidogo pombe, soda, jamani mbona wana mabilioni ya pesa wanayaacha, hawaoni kama wana uchumi mkubwa wanauacha? Wanatuweka Tanzania katika hali ngumu, lakini kumbe hali ya kupata uchumi ipo. Tujiulize, kwani wataalam wanafanya kazi gani? Uchumi huu wanaoukalia wanafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike mahali basi tuambiane ukweli kama tumefeli tuseme tumefeli; kama hatujafeli mambo matatu nataka yatekelezwe. Suala la pato la mjusi, suala la Selous na suala la wawekezaji wa ndani kupewa kipaumbele ikiwemo A to Z ya Arusha. Wameweka Mwekezaji, amekuwa frustrated hata kufunga kiwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengine nakushukuru sana dakika tano zimenitosha.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani za dhati. Nakushukuru kwa kunichagua na mimi kuwa mmoja wapo wa kuchangia siku ya leo. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na nitoe pole za dhati kwa Watanzania wenzangu na wananchi wa Mkoa wa Lindi hasa katika Wilaya ya Kilwa kwa kifo cha Mzee wetu Kingunge Ngombale Mwiru, Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niangalie Tanzania kwa ubora wake na jinsi Mwenyezi Mungu alivyoipendelea. Ameipendelea Tanzania kwa kuturuzuku vitu mbalimbali ikiwemo mito mikubwa unaikuta Tanzania. Tanzania ni nchi ya kumi na moja kuwa na vyanzo vikubwa vya maji ikiwemo Maziwa ya Victoria, Tanganyika, Nyasa, mito mikubwa tumeipata Tanzania lakini Mwenyezi Mungu akatujaalia tukapata bahari Tanzania, hivyo hata tukisema mizigo inateremshwa Tanzania, nchi za wenzetu wanashindwa kupata vitu kama rasilimali ambazo tumepata Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumeruzukiwa mbuga kubwa za wanyamapori na urithi wa dunia tumeupata Tanzania ikiwemo Kilimanjaro, Serengeti, Selous Game Reserves na nyinginezo. Mwenyezi Mungu bado akaendelea kutusaidia sisi kutupa madini ya kutosha. Sasa hivi Tanzania nzima kila mkoa unaokwenda kuna madini. Kuna madini ambayo hata nchi zingine hawana kama Tanzanite, lakini tunajiuliza bado Tanzania wananchi ni maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajiuliza tumekwama wapi mpaka Watanzania tumekuwa maskini namna hii? Suala hili tujiulize Watanzania wote kwa uchungu wa nchi yetu kujiuliza kwa pamoja sio kumwacha mtu mmoja anakimbia peke yake, huku nyuma watu wamemwachia anachokifanya peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuziona resources kama hizo ambazo Tanzania zinachezewa chezewa nataka niongee katika zao ambalo liko katika Mkoa wangu wa Mtwara na Lindi. Hili ni zao la korosho. Zao la korosho sasa hivi limezagaa Tanzania nzima, lakini cha kushangaza baadhi ya wananchi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara na baadhi ya mikoa wanayolima korosho kufaidika katika kipindi cha miaka miwili na nusu kutoka korosho Sh.600 mpaka kufikia Sh.4,000. Kinachoshangaza sasa hivi kumetokea sabotage kubwa sana katika hili zao za korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimuachia nyani shamba utavuna mabua na usipoziba ufa, utajenga ukuta. Tunajua kabisa haya ni mambo yanafanyika na Serikali inasema ina mkono mpana, huu mkono mpana uko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, korosho kama korosho Tanzania haionekani pamoja na kwamba sisi ndio tunaolima korosho. Inaonekana ya kwanza Vietnam; ya pili, India; ya tatu Nigeria; Ghana, Brazil, lakini Tanzania hatupo. Wafanyabiashara wakubwa wa korosho wanakuja kununua korosho Tanzania. Ametokea Vietnam kuja kununua korosho Tanzania amekutana na mazingira magumu sana ya kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya kwanza wali-hold makontena yote akajikuta ana korosho imekaa katika warehouses hawezi kuziondoa, hivyo anaanza kufanya biashara yake kwa hasara, mpo Watanzania? Sasa hivi tumeyaona, mimi nilirusha clip kwa Wabunge kuwaonesha jinsi korosho za Lindi zimetiwa mawe, kokoto, mchanga zimezunguka tayari ziko Vietnam korosho zetu ambazo zimewekwa mchanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnasema mna mkono mpana, mkono mpana uko wapi hapo? Kama ni hivyo, hata mimi nina mkono mpana, kama kwa mkono wenyewe namna hii kujikuta mazao yetu yanapelekwa India, yanapelekwa Vietnam yakiwa na kokoto ni aibu kwa Taifa na uchumi huu utadorora kwa vile kuna kundi la watu hawataki kuona Watanzania wanafanikiwa, hawataki waone katika Tanzania hii wananchi wa Tandahimba, Naliendele, Mchinga ambao sasa hivi walikuwa wanaweza kupata milioni 50, hawataki, wanataka kuturudisha nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu isilitazame suala hili kwa kawaida, ilitazame suala hili kwa mapana yake. Wewe ni shahidi, tupo humu ndani kwa muda mrefu, tulikuwa na viwanda vya korosho, viko wapi? Humu ndani tunasikia maneno, tutafufua, tutafufua! Viko wapi? Bado wamevishika, wamevifunga, hawajavifufua, viwanda hivyo wananchi hawana ajira na wao wanafanya kazi zao kwa sababu hawaoni thamani na viwanda vile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda 13 viko wapi? Masasi kulikuwa na viwanda, Newala kulikuwa na viwanda, Lindi kulikuwa na viwanda, Dar es Salaam kulikuwa na viwanda mpaka leo havijafufuliwa, viko wapi viwanda? Halafu mnasema mtakuja mtuletee viwanda tena, vile mlivifanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wananchi wanatafuta ajira, kwa vile korosho mnapeleka India, ajira inakwenda India! Sisi hatuonekani kama producer wa korosho, Watanzania tuko katika aibu kubwa. Kahawa ya Tanzania inauzwa Uganda, sisi wenyewe tuko wapi? Mazao ya Tanzania yanauzwa Kenya, ina maana Kenya they are strong enough kusimamia mazao yao na maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na natural resources tulizokuwa nazo Tanzania tumepitwa na nchi zote tunazoziona, Kenya, Uganda, mpaka Rwanda imetupita, Tanzania ya mwisho. Tujiulize tumerogwa na nani? Mtanijibu mtasema tena wewe, basi tumejiroga sisi wenyewe kwa kuwakumbatia watu ambao wana-sabotage uchumi wetu lakini tunawaangalia kwa sababu ya maslahi binafsi na corruption. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PIC. MSD wamekuja katika meza yetu na baadhi ya Taasisi nyingine, MSD wamebuni tenda ya ku-supply dawa nchi 15, sheria zilizokuwa mbovu za Tanzania, feasibility study tu inatakiwa ifanyike kwa muda wa mwaka mmoja, strategic plan one year, action plan one year... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti,Bismillah Rahman Rahim.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza na Mwenyezi Mungu anijalie hilo nitakalolizungumza liwe ni haki na ukweli. Tukisimamia haki tutafikia mahali ambapo nchi hii tutaitendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge inabidi turudi Majimboni kwetu tukawaombe radhi wananchi wetu. Bunge hili ndilo tulipitisha haya mambo, lakini leo wanaichukulia hii hoja kuwa ni hoja ya sehemu moja, kuona wao ndio wana hoja hii, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie kitu na Wabunge wote wanielewe, tuliapa kwa kushika Quran, tuliapa kwa kushika Biblia, hivi vitabu ni vya Mwenyezi Mungu na vitabu hivi havitakiwi kudanganya na kuvifanyia uwongo, mbele yetu kuna Mwenyezi Mungu. Unapoishika Biblia ukasema naapa na kumtanguliza Mungu katika Biblia halafu ukaja hapa ukazungumza uwongo ni dhambi kubwa, inabidi tukaombe radhi hiyo kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unashika Quran, ukasema naishika Quran kwa kuahidi na kuilinda kwa mujibu wa Sheria na Katiba halafu baadaye ukaja kuibadilisha kwa kuzungumza vingine hii ni laana kubwa. Kila siku unasema tumerogwa na nani? Imeturoga Quran, imeturoga Biblia. Mara nyingi ukiwa mkweli, unakuwa hukubaliki mahali popote pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ni shahidi ni Mwenyekiti kipindi cha tatu hapa ndani na baadhi ya Wabunge tupo ndani kwa muda mrefu tunayaona haya.

Hata hivyo, kuna wakereketwa na wanaharakati walionyesha hii hali kuwa hali ya madini ni ngumu, nataka niwataje kwa majina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla Ubunge wake ulikuwa wa tabu kwa vile aliyasimamia kwa dhati kuhakikisha madini haya hayaharibiwi wala hayachakachuliwi, alipigwa mabomu, akadhalilishwa inabidi aombwe radhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kafulila alisimamia kwa dhati akaitwa tumbili humu ndani. Mheshimiwa Zitto Kabwe alikuja na hoja nzito ambazo zina mashiko lakini siku ya mwisho ndio inakuwa hapana na hapana inakuwa ndiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Rais ameonesha ushujaa kwa kukubali maamuzi na matakwa ya Wanaharakati hawa na akayafanyia kazi ndiyo hayo unayoyaona maamuzi mazuri yanakuja sasa hivi. Hivyo siyo hoja ambayo imeletwa na upande mmoja, hii ni dhambi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa Mjumbe wa Kamati ya Nishati na Madini, jina nililopewa ni jina la sura pana, mnalikumbuka au hamlikumbuki Wabunge? Maana yake nilikuwa nasema kuna baadhi ya Wachina walikamatwa Arusha na madini ya Tanzanite ikasemekana hawajui Kiswahili na Kiingereza, wakaachiwa yale madini. Tulikuja kuhoji hapa ndani mwisho wa siku tukasema ndio akapita Mchina akaenda zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walikamatwa Wachina na pembe za ndovu Rukwa, shahidi ni Mheshimiwa Jenista Mhagama nilikuwa naye katika ziara. Lori la pembe alilokamatwa nalo yule Mchina ikasemekana hajui Kiswahili na Kiingereza, Mheshimiwa Jenista ni shahidi na tulikuwa na Mheshimiwa Lekule Laizer, lakini mwisho wa siku tukasema ndio na hapana ikawa hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifikie mahali, juzi nilitoa taarifa nikasema mtakuwa tayari wenzetu penye ndio kusema hapana? Maana yake msiburuzwe kwa ndiyo wakati kuna hapana ndani yake. Kulikuwa na baadhi ya Wabunge walikuwa wanaona hiki kama tunachokifanya hiki ni dhambi kwa wananchi, sasa leo mnailetaje hoja hii ikawa ni hoja ya upande mmoja? Haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hoja ni ya Magufuli na wanaharakati na msiichukulie kama hoja ya kisiasa Wabunge wote iwe wa Upinzani, iwe wa CCM tushirikiane kwa hili. Unapoleta uchumi bora, huleti kwa upande mmoja ni kwa Watanzania wote, leo tunaiona Bulyankhulu watu ni maskini, unaiona Geita watu ni maskini, lakini umaskini huu umesababishwa na mikataba yetu mibovu na sisi wenyewe kusema ndio wakati ni hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge tumeumbuka, kwa aibu hii hatuna haja ya kufumba macho na kupepesa macho, tuwaombe radhi wananchi. Narudia tena Wabunge tumeumbuka kwa hili, hakuna haja ya kupepesa macho, wala kumwambia mwenzako kumkodolea kwamba ni hoja ya CCM au hoja ya CUF au hoja ya CHADEMA, ni hoja ya Wabunge wote tumekosea humu ndani. Watu wengi walikuwa wanaangalia conflict of interest na conflict of interest ikajengea hoja tunaitana pembeni jamani tukubali, wakati unajua kabisa hiki ni hapana, hizi ni dhambi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa idhini ya Sheria za Bunge tutoe hii Kanuni ya kushika Quran na Biblia itatulaani humu ndani. Tunashika Biblia wakati Biblia haitamki uwongo, tunashika Quran haitamki uwongo, leo tunatamka uongo halafu baadaye tunakula matapishi, tunageuza leo, tunabeza na kukebehi na kuona wenzetu hawana hoja. Nani humu ndani atamwomba radhi Mheshimiwa Kafulila? Nauliza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba radhi Kafulila kwa vile Mheshimiwa Kafulila ameonewa wakati alikuwa analeta hoja ya kuisadia nchi hii. Tulikuja na hoja ya Tanzanite,

Tanzanite inatoka Tanzania, mimi nilikuwa New York pale karibu na UN nje kuna maduka ambayo yanauza madini, Wallah Tanzanite hiyo inaonekana inatoka Kenya, inatoka India, inatoka South Africa, niliuliza kwani hakuna Interpol? Jibu halipatikani, lakini leo hapa watu wanataka kufumua mapafu kuzungumza uwongo, dhambi kubwa sana na itatulaani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimshukuru na nimpongeze Rais Magufuli kwa vile amethubutu na sisi wote tuungane kwa pamoja bila unafiki kumpongeza kwa kazi anayoifanya kubwa na inahatarisha maisha yake. Hivyo kila Mtanzania amwombee huruma kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hapo nakuja katika hoja iliyopo mezani. Leo tunasema tunataka uwekezaji wa viwanda, katika viwanda tumeona A to Z imekuja kufanya semina ngapi hapa ndani? Wanakuja wageni wanaingiza vyandarua bure, hawana tozo, yeye analipa bilioni 17 wale watu wameachiwa vilevile waingize vyandarua hakuna mahali palipobadilishwa hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri wa Fedha tulikuwa naye katika semina ,akasema atalifanyia kazi, lakini nimeangalia katika vitabu hawa A to Z wameachwa hivi hivi, kiwanda chao kinakufa, wanalipa kodi, wana madeni na marekebisho hayajafanywa. Naomba Serikali hii kama tunavyosema ni Serikali sikivu iangalieni A to Z ili angalau yale maombi yao yasikilizwe yafanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko humu ndani ya Bunge miaka mingi tumezungumzia suala la Dinosaur. Dinosaur yupo Ujerumani sisi hatutaki mjusi aje Tanzania lakini je, hata mrabaha haiwezekani? Tunakimbizana na mama lishe, tunakimbizana na watu wa mitumba, leo kuingia ndani ya exhibition unatoa Euro 24 kwa watu wazima na Euro 12 kwa vijana lakini watu wa ndani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nakushukuru. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema nami kuchangia katika hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tunahitaji amani na amani haichezewi. Watu wanajaribu kuangalia ubinafsi bila kuiangalia nchi inakwenda wapi. Popote panapotokea vita wahanga ni wanawake na watoto. Leo wanasema usipoziba ufa utajenga ukuta. Tumeiona Libya sasa hivi wanawake na watoto wanahangaika. Tumeiona Iraq, wanawake na watoto wanahangaika, tunaiona Somalia, wanawake na watoto wanahangaika, tumeiona Rwanda, wanawake na watoto walihangaika, wanakuja mpaka Tanzania kama wakimbizi na Burundi hivyo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzo chokochoko ndogo ndogo zinazoanza ziwe za kidini, ziwe za kisiasa. Wachungaji, Maaskofu na Mashehe watangaze dini. Nia ya kupewa nafasi hiyo kutangaza uadilifu, kuitangaza amani kwa wananchi wao. Wakianza Maaskofu, Mashehe kujiingiza katika siasa, siasa ni propaganda. Sasa wanataka kutangaza mchezo wa propaganda waingize katika dini, haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Serikali isimamie kikamilifu. Kwa mfano, mimi hapa mlemavu, ikianza vita mtakimbia humu nyote, mtaniacha mimi niko humu ndani. Hivyo mhanga namba moja ni mlemavu. Wagonjwa waliokuwa mahospitalini watakuwa wahanga wa vita. Wazee watakuwa wahanga wa vita. Watanzania hatutaki vita. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, kama wana hoja, iletwe hoja patafutwe ufumbuzi na usuluhishi. Kutumia majukwaa ya dini kutangaza mazungumzo ambayo yatawafanya vijana wapate mihemko, waingie mtaani wafe wao wakimbie, haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi kuna clip ya mtoto amekimbia Syria, ameokotwa na UN ameshika nguo ya mama yake na dada yake, anasema nakwenda kumshtakia Mungu, mama yangu anauawa namwona hivi hivi, baba amekimbia. Wanaume hawana uvumilivu na watoto. Pakianza vita, wanaume wote wanakimbia wanaacha akinamama wanahangaika hapa. Wanawake Tanzania nzima, tuungane tupinge hii kitu. Tutakaoathirika ni wanawake. Haikubaliki na wala haitakubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunashiba kwa vile pana amani hapa. Tunataka maji hapa kwa vile pana amani. Mnataka barabara kwa vile pana amani hapa. Bila amani hakuna maji wala barabara. Bodyguard anamkimbia Rais, bodyguard anamkimbia Waziri Mkuu, kila mmoja anatafuta taharuki, anakimbia anakwenda anakokwenda kwake. Tusilichukue kama ni kitu cha mzaha, ni kitu hatari. Watanzania nimewaangalia leo nilikuwa nasikiliza hotuba ya Mheshimiwa Rais Nyerere akisema hivi: “Kuna watu wanaangalia maslahi ya mabepari na kuna watu wanaangalia haki za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hao wanaoangalia haki za mabepari waangaliwe kwa macho mawili ili wasituingize katika mgogoro.” Hata hiyo amani isimamiwe kwa ukamilifu. Kama kuna wanaovunja amani upande huu na upande wa pili vile vile ushughulikiwe. Msumeno unakata mbele na nyuma, haukati sehemu moja. Italeta furaha na faraja kuona wale wanaotaka kuleta uharibifu wa amani nchi hii wanashughulikiwa bila kuangalia anatoka wapi? Anaelekea wapi? Amani ni amani tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie miradi na mikopo ya Tanzania. Kwa muda mrefu Tanzania ina madeni makubwa, tena madeni makubwa sana lakini madeni haya yalisababishwa na mikataba ambayo haikufanyiwa analysis. Nitatoa mfano, anakuja World Bank, anatoa mradi wa Selous, ule mkopo nitalipa kwa miaka 25, lakini anakupa condition ambayo badala ya kusema utafaidika, anafaidika yeye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walikuja kututawala, sasa hivi wanatutawala kwa kupitia mikopo. Mkopo wa shilingi bilioni 500 anakwambia utalipa kwa miaka 25. Kila mwaka kwa maana hiyo nitalipa shilingi bilioni 20. Shilingi bilioni 20 nikichukua mwakani riba inarudi pale pale mpaka miaka 100 mkopo huo hauishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile wao wanacheza na akili yetu bila kuangalia sisi wenyewe kama hicho wanachokifanya kina usahihi gani katika kufanya analysis? Analeta mkopo wa shilingi bilioni 500, anaweka na conditions za pembeni. Watakuja kufanya kazi ma-expatriate wetu, watalala katika nyumba kubwa, wanataka wafanyakazi wanne, mshahara wake kwa mwezi dola 20,000; kila mwisho wa mwezi atakwenda Mikumi au Serengeti. Ile mikataba ya pembeni ukiisoma inatia kinyaa kabisa. Haiifanyi nchi hii kama itaweza kukwamuka kwa kupitia hii mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jiulize, ilijengwa reli ya kati, kutoka Kigoma mpaka Dar es Salaam kwa kodi za vichwa za Watanganyika wakati ule. Kila Mtanganyika aliambiwa atoe kodi; na waliijenga reli kwa hela zetu kutoka Kigoma mpaka Dar es Salaam. Matokeo yake ilikuwa ni wao kuja kuchukua madini, wao kuchukua pembe na wamefaidika wamekuwa matajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutajirika, wamekuja na system ya pili ya mikopo. Naomba, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni mwenye dhamana na Mawaziri, waiangalie mikopo kwa umakini sana. Nina imani kuwa hii kazi ndugu yangu anaiweza. Awaokoe Watanzania ambao wanaangamia na mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkopo wa Selous, umeletwa mkopo maeneo ya Udzungwa, Mikumi na Ruaha, zote ziko chini ya TANAPA. Wanataka kujenga viwanja vya ndege, barabara kutoka Lindi kwenda Liwale hakuna. Kwa nini wasituambie tunataka mkopo huu ukajenge barabara ya Liwale ili watalii waende Liwale? Kwa nini wasijenge barabara ya kwenda Namtumbo ili watu waende Namtumbo? Wanatupa conditions ambazo zinatufanya tunakwazika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mradi huu utapita, najua kweli hii Serikali siyo sikivu na nitaufuatilia. Kama Serikali ni sikivu, mkopo wa World Bank unaokwenda Selous ufanyiwe kazi ili mwananchi wa mikoa mitano hii ikiwemo Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma ambayo tumeiacha kwa muda mrefu kwa miradi mikubwa, kwa kweli sitakubaliana nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na mradi wa SAGCOT. SAGCOT ni Sothern Agriculture Corridor of Tanzania. Lindi, Mtwara na Ruvuma tuliachwa. Hii ni mikakati ya makusudi ya kutufanya Mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma tuendelee kuwa maskini. Sasa wamelala waliolala, sisi bado tuko macho. Ndiyo maana Mwenyezi Mungu ameturudisha tena kuja kuangalia haya, je, wataendelea kutukandamiza Mikoa ya Kusini? Kama unataka kuleta msaada wa utalii kusini, unaiachaje Kilwa, wakati Kilwa katika heritage ilikuwa namba 21? Naomba mradi huu wa World Bank utushirikishe Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma kwa kikamilifu ili tuwe beneficiary kwa mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia barabara. Hata Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi katika kutembelea mikoa yote; Mikoa ambayo iko nyuma ni Lindi, Mtwara na Ruvuma katika barabara. Sasa uwiano wa maendeleo, kuna wengine wanapaishwa kwa maendeleo, wengine wanawekwa nyuma, haikubaliki. Watanzania ni Watanzania wote tunahitaji kula hii keki. Leo Mkoa wa Lindi, Mtwara na Ruvuma tuna produce korosho ya kutosha; uchumi wa nchi uko juu; leo umwambie mtu twende Liwale, hawezi kufika. Mwambie mtu aende Milola sasa hivi hafiki. Hakuna barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba bajeti itakayokuja ya Wizara ya Ujenzi iangalie mikoa ambayo imeachwa kwa muda mrefu ipewe priority. Hii itatufanya na sisi tufarijike kujiona na sisi tuko ndani ya keki ya Watanzania. Tunawaona wenzetu Kaskazini wanavyosaidiwa huko, nasi tunataka Kusini iende sambamba na mikoa mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengi, nimekuja kuzungumza hayo machache kuitangaza amani, amani hii itatusaidia katika kilimo, afya na elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nawashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijaalia nami kuchangia hoja iliyopo mbele yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe shukurani za dhati kwa Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Naibu waziri na Dkt. Mseru na Dkt. Mgassa. Mnamo mwezi Machi, kulikuwa na mtoto anaumwa sickle cell akawa na damu mbili nikapigiwa simu saa tano kwamba hali ya mtoto yule ni mbaya na huyo mtoto ni Rais wa ugonjwa wa sickle cell Africa. Nilimpigia Mheshimiwa Ummy usiku saa sita akanijibu na alitumia uwezo wake na huruma yake na yule mtoto aliongezwa damu, sasa hivi yule mtoto anaendelea salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Dkt. Mgassa alikuwa nje ya nchi, baada ya kupata taratibu zile alimtafuta Dokta. mwingine ambaye alikuwa yuko Dar es Salaam mpaka saa 7.30 usiku yule mtoto ameweza kuongezewa damu lita kama nne hivi nafikiri na yule mtoto anatoa shukurani za dhati kwa niaba ya familia yake, Mheshimiwa Ummy na wote wahusika Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa mzima nikiwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano, nikapata ajali, sasa hivi mimi ni mlemavu. Mtu ambaye amenisaidia sana ni Dkt. Mseru Mwenyezi Mungu ambariki sana. Hivyo, kwa niaba ya Madaktari wote, naomba Dkt. Mseru anifikishie salamu zangu za dhati, Mwenyezi Mungu awajaalie Madaktari wote Tanzania kwa huruma na kazi ngumu wanazofanya kwa kuwasaidia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mwenyekiti wa kupambana na malaria ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mimi Riziki Said Lulida niko tayari kutokomeza malaria Tanzania wewe je? Twende zetu Kasulu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tuna ugonjwa hatari wa malaria na malaria inaua, lakini nataka nitoe kitu kimoja ambacho nimekiona kwa muda mrefu kutokana na uzoefu niliokuwa nao. Malaria ni ugonjwa hatari lakini kuna wafadhili wanasema wao wanatoa fedha kwa ajili ya kusaidia malaria, hizi pesa hazionekani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Waziri Mkuu kwa vile yeye ndio mdau katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na wenzake nataka watujibu hizi pesa za malaria zinakwenda wapi? Nimeweza kuhudhuria mikutano mingi ya mararia ikiongozwa na USAID na Taasisi nyingine wanasema tumepeleka Tanzania bilioni 600 zinakwenda wapi hizo pesa. Mimi sijajua mpaka leo na nimejaribu kumuuliza Naibu Waziri ananiambia hata na mimi vilevile Mheshimiwa Riziki hatujui pesa za malaria zinakwenda wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, malaria kama hizi pesa ambazo wanasema wanatuletea hazijulikani zinakwenda wapi, mimi napata kigugumizi na kujiuliza kuna nini na hizi pesa za malaria. Kwa mfano, pesa za UKIMWI zinaonekana ndani ya halmashauri, katika halmashauri tunaweza tukazikagua zile pesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kuna hela za Global Fund, kuna hela za TACAIDS, kuna hela za Bill Clinton, Kuna hela za Foundation ya Benjamini Mkapa zinaingia ndani ya halmashauri na zinaweza kukaguliwa. Hizi pesa za malaria naomba Waziri mwenye dhamana aniambie ziko wapi ili tuweze kuzifanyia kazi na Watanzania waweze kuzitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, malaria yalikuwa yamepotea lakini sasa hivi malaria imeongezeka kwa kiasi kikubwa. Mikoa ambayo ina malaria ni mikoa ya kanda ya ziwa ikiwemo Geita, Simiyu, Mara, Kigoma na Lindi na Mtwara. Sababu za msingi za kuwepo maeneo hayo malaria ni kwa ajili ya migodi mikubwa ambayo iko katika hiyo mikoa wameacha mahandaki makubwa, lakini mahandaki haya yalisababishwa na mikataba mibovu ambayo EIA haikufuatwa, hivyo baada ya kumaliza machimbo wameacha machimbo yakiwa wazi na mbu wamezaliana kwa wingi hiyo mikoa sasa hivi iko katika hatari kutokana na malaria.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba suala hili la malaria lisimamiwe kwa kikamilifu ili wananchi wa Mikoa hiyo Geita , Simiyu, Mtwara, Lindi, Kigoma, Katavi tutakuwa tumepoteza watu wengi hasa wanawake na watoto, wajawazito ndio walengwa wakubwa wa malaria.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia suala la NHIF bima ya afya ni mkombozi kwa Watanzania na ilichukuliwa bima ya afya bima ikawa ni kwa ajili ya wafanyakazi wa Serikali na taasisi zake, lakini walisahau kama kuna wakulima wanauza mazao na hao wakulima wanapouza korosho wanapata pesa kama milioni 50 wengine milioni 20, naomba watu wa bima ya afya itengeneze mikakati maalum ya kuhakikisha hata wakulima na sekta binafsi ziwe zinatoa msaada na kuweza kulipia bima ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nazungumza hivyo Wabunge kila siku unapigiwa simu, mimi naumwa nataka kwenda Dar es Salaam lakini kama angetengenezewa mazingira mazuri ya korosho zake, kuwa unapouza korosho unatoa bima ya familia ya milioni 1,500,000, matatizo haya yangeweza kwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wavuvi wanavua kanda ya ziwa dagaa, Zanzibar wanavua kila kitu, wanapata pesa, je, ni mikakati gani wametengeneza ili watu wale wanawatembelea na kuweza kujiunga na bima ya afya. Mambo ya kuwa tegemezi kutegemea wafadhili, wafadhili sasa hivi wamekuwa kama wanatubabaisha, wanatunyanyasa leo nitatoa kesho sitoi. Mazingira haya ya kutegemea wafadhili ni aibu kwa Taifa tutumie njia ya sisi wenyewe kuweza kujitegemea na sio kutegemea watu wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona tunaweza kutokomeza malaria kwa kutumia pesa zetu za ndani. Hatukatai kuchukua pesa za nje, lakini pesa za nje sasa hivi zina masharti ambayo yanatufanya tunakwazika, tunakuwa na madeni mengi ambayo tukijiuliza hela hizi kama hazisimamiwi, ni mzigo mkubwa kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia damu salama kwanza nataka nilete hamasa kwa Wabunge tuchangie damu salama. Ugonjwa wowote ni utarajiwa hautegemei wakati wowote, unaweza kupata ajali ukategemea upewe damu, unaweza ukajikuta mwanao anaumwa, familia yako inaumwa ,hivyo suala la damu salama lipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niwashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia nami kuchangia katika hoja iliyopo mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiona mahali Waheshimiwa Wabunge wanaliongelea eneo hilo basi Serikali ilifanyie kazi. Waheshimiwa Wabunge wengi wanaongelea TRA. Sasa hivi TRA ni eneo ambalo haliko rafiki na wafanyabiashara wadogo wadogo. Wameweka urasimu wa makusudi, siwezi nikasema ni wote, lakini maeneo mengi ya TRA sasa hivi ni eneo ambalo linawakwamisha wafanyabiashara wadogo wadogo, hivyo, siyo eneo rafiki kwao. Hili eneo litawakatisha tamaa wafanyabiashara hawa ili wasiweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyosikia, unatakiwa kwanza wakutoze ushuru hata kazi hujafanya. Mama Ntilie anapika wali, hajajua kama anaweza akauza wali wake, umeshamwekea tayari, lipa shilingi milioni moja, anaipata wapi? Huu ni unyanyasaji wa kibiashara kwa wazawa.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kwenda katika Tanzania ya viwanda. Tanzania ya viwanda inahitaji mazingira wezeshi kwa viwanda. Enzi za Mwalimu Nyerere alianzisha maeneo ya viwanda na maeneo yale aliweka mazingira mazuri ya maji, umeme na barabara. Kwa mfano, alianzisha viwanda 14 vya korosho, hili nalirudia tena karibu mara ya tatu, viwanda vile vilikuwa na umeme, maji na ajira ya kutosha. Vilevile walikuwa wana uwezo wa kupata malighafi ya korosho palepale katika mikoa inayozalisha korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimeona katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ametaja mikoa yote ambayo imepewa kipaumbele cha viwanda; Lindi, Mtwara na Ruvuma sijaiona hapa. Kwa maana moja, hata hivi viwanda vya korosho vilivyopo, mategemeo ya kuvifufua hayapo. Ni aibu kiasi gani korosho inalimwa Tanzania inanunuliwa inapelekwa India, wanakwenda ku-process tunaletewa korosho ile iliyobanguliwa kuja kula tena Tanzania. Huu siyo mfumo mzuri wa kibiashara. Tunavyo viwanda vya korosho Tanzania lakini unavikuta vinapeleka korosho nje ya nchi as a raw material. Huu ni uharibifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda katika semina ya korosho, tunaambiwa Tanzania haionekani kabisa kama ni mzalishaji wa korosho, kwa vile tunaipeleka nje wale ndio wanaonekana wanazalisha na kusafirisha korosho. Je, tutapata lini ajira kama korosho yote tunaipeleka nje? Viwanda vyote vimefungwa. Cha kusikitisha zaidi, Mkoa wa Lindi hatuna kiwanda hata kimoja. Hivyo viwanda vya korosho vilivyokuwepo; vya Mtama na Lindi, vyote vimefungwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama Mheshimiwa Waziri ameikutia tu hii issue, ni makosa makubwa yalifanyika ya ubinafsishwaji na uwezeshaji. Uwekezaji wa nchi hii haukuweka mazingira mazuri katika mikataba, haukuweka mazingira mazuri kwa kujua nini tufanye katika kubinafsisha. Tumewabinafsishia watu, wamevifunga viwanda, watu walewale ndiyo wanapeleka korosho nje. Haiwezekani kabisa. Nataka utupe taarifa, ni nani wamechukua viwanda? Bado walewale waliochukua viwanda wanapeleka korosho nje, huu ni uhujumu wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na viwanda Tanzania ambavyo vinakamua mafuta. Mwanza tulikuwa tunapata Mafuta ya OKI, SUPA-GHEE, TanBond ya Tanzania ambayo hata Kenya walikuwa wanaipeleka, viwanda vile vyote vimefungwa, kwa nini vimefungwa na nani amevifunga? Kama ni mkataba, mkataba wake ulikuwa wa muda gani? Palikuwa na mikataba mibovu ambayo haikuwa na timeframe. Hivyo mtu amechukua kiwanda, amekifunga, anaagizia mafuta machafu kutoka nje wakati tunaweza kutengeneza mafuta masafi Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki ni nini? Nafika mahali sielewi kama najielewa au pengine mimi niko nyuma ya wakati. Viwanda vya mafuta tunavyo. Nachingwea tulikuwa na viwanda vya mafuta, Mafuta Ilulu, ufuta wetu wote ulikuwa unakamuliwa Nachingwea. Leo ufuta wote wa Tanzania tunaupeleka nje, halafu hapa tunalalamika tuna uhaba wa mafuta wakati mafuta yetu mnapeleka mbegu nje, mnapeleka ajira nje na raw material inabakia kule na makapi yanatengeneza feed cake za wanyama. Huu ni uhuni wa kibiashara ambao umechezwa kwa muda mrefu, tunafanya biashara kwa mazoea, matokeo yake tunaiweka nchi katika crisis. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila inapofika karibu na Ramadhani wafanyabiashara wanaanza uhuni wao; mara hakuna mafuta, sukari, hii ni crisis ya makusudi wanataka kupandisha bei ili wananchi wapate ghadhabu na Ramadhani. Mfanyabiashara kupata pepo ni ngumu sana. Wanaangalia ni eneo gani nitafanya fujo yangu halafu watu watahamasika ili angalau hili litakuwa ni chachu kwa wananchi kulalamika hakuna sukari na mafuta. Nina imani sukari ipo, mafuta yapo, yatafutwe na wananchi wapate sukari na mafuta. Tumechoka kusikiliza uhuni wa kibiashara wa muda mrefu. Nchi haiendeshwi kwa uhuni wa kibiashara, nchi inaendeshwa kwa taratibu zilizopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii alizeti inapelekwa nje, magazi kutoka Kigoma yanapelekwa nje, wanachuja wanatuletea tena, ooh, tuna mafuta yako nje yamenasanasa. Kwa nini mmefunga viwanda vyetu vya mafuta na mmevizuia hamkamui mafuta, mnatuletea matatizo kibiashara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika sana kusema ubinafsishaji ndiyo donda ndugu la nchi hii. Tumefunga viwanda vyote. Tulikuwa na viwanda vya kusokota nyuzi. Kamati ya PIC tulikwenda Ubungo, eti hata nyuzi tunaagiza kutoka China. Tulikuwa na viwanda vya kusokota nyuzi Tanzania, pamba inatoka Mwanza na Shinyanga. Wenzetu, ndugu zetu, watani zangu Wasukuma wanalima pamba, ile pamba inabidi ipelekwe nje ikatengenezwe nyuzi tuletewe Tanzania wakati tulikuwa na viwanda vya nyuzi, tulikuwa na Kiwanda cha Mwatex na Kiwanda cha Kilitex. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, yeye ni mbuzi wa kafara, haya mambo ameyakuta. Naomba timu nzima ya Mawaziri irudi ikakae ituambie viwanda hivi viko wapi, vinafanya nini? Tupate database, nani wamechukua na kwa nini wanatuletea crisis ya mambo ya viwanda? Haiwezekani kila siku tunachukua khanga mbovu kutoka nje, madira mabovu kutoka nje, wakati Tanzania tulikuwa tunatoa khanga nzuri; Kenya na Uganda soko kubwa lilikuwa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kusema sana lakini najiuliza, kulikoni Tanzania? Tumekuwa katika zigizaga, nenda mbele rudi nyuma, nenda mbele rudi nyuma. Viwanda hivi kwanza vingefanya kazi, basi hivyo vingine vingekuwa vya ziada kwa vile tayari ajira na uchumi ungekuwa mkubwa, lakini vile viwanda vikubwa vyote vimefungwa, kwa nini? Nani amevifunga, ni hao hao wafanyabiashara. Nataka utakapokuja kesho, uniorodheshee majina yote ya waliochukua viwanda na mpaka leo wamevifungia. Kwa nini wamevifungia na kwa nini nguo hazitengenezwi Tanzania? Kwa nini nyuzi hatusokoti Tanzania? Kwa nini korosho tunapeleka nje, tunaletewa tena zile zile hapa Tanzania? Kwa nini ufuta mnapeleka nje na tunakosa mafuta Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina mengine ya kusema, nataka jibu hilo kesho. Ahsanteni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia na mimi kuchangia katika hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka ni-declare interest kwamba mimi ni Mwenyekiti wa Kupambana na Ujangili na Kusimamia Uhifadhi ndani ya Bunge na Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla alikuwa Katibu wangu katika taasisi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru nilipata nafasi ya kuizungukia Tanzania nzima katika masuala ya uhifadhi na kuangalia mwenendo wa ujangili Tanzania, kwa kweli nimejifunza mengi. Niliomba katika Bunge lililopita, Wabunge walishiriki kuzunguka kutembelea Selou, akiwemo Mheshimiwa Keissy, Mheshimiwa Susan Kiwanga, waliyoyaona na yanayozungumzwa Bungeni mengine mengi ni ya uzushi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia masuala ambayo mimi nimeyaona na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi na ndiyo maana namuomba Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, atoe fursa Waheshimiwa Wabunge wazunguke wakaone haya yanayoonekana kuhusu mifugo, masuala ya mipaka watakuja na uelewa tofauti. Kuna wengine watakuwa wanafuata mtu ameongea nini na yeye anafuata mkumbo wa kuongea lakini ukienda kuangalia kiuhalisia mengi yanayozungumzwa utaona si ya ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru Pato la Taifa katika suala la utalii limeongezeka kwa asilimi 17.6. Huu ni uchumi ambao tunaotegemea na katika maeneo ambayo tunafaidika ni TANAPA na Ngorongoro, upande wa uwindaji mpaka leo pamekuwa na utata. Sasa watu wanaangalia uwindaji lakini mnapata nini, wanyama wanakwisha, wanyama wanatoroshwa, matokeo yake mnatetea uwindaji ambao hauna faida. Inabidi tusimame pamoja tuangalie kandanda ya uwindaji kuna nini? Maana tumewamaliza wanyama Selous, corridors zote zimekuwa intervined binadamu lakini leo ukiangalia katika hunting kuna nini ndani ya hunting, hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua tathmini leo nitakwambia TANAPA wameingiza shilingi bilioni 237 na wamepeleka Serikalini kama ruzuku shilingi bilioni 37 lakini huwezi kupata jibu katika uwindaji. Nitakwambia Ngorongoro walichokipata na walichokipeleka Serikalini, lakini leo utajiuliza TANAPA kwa nguvu zote inazozifanya hapa Serikali imeshindwa kuisaidia TANAPA ili iweze kujiendesha kwa mwaka mzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, inatoa asilimia 15 kupeleka Serikali, inatoa asilimia 30 TRA lakini akijenga barabara inabidi alipie ushuru, akipeleka umeme analipa ushuru na asilimia 3 inakwenda Kurugenzi ya Utalii lakini wenyewe wanashindwa hata kuzunguka kwenda kufanya promotion na marketing ya TANAPA yao. Huwezi kumuachia mwenzako akutangazie, ni lazima na wao wenyewe waende wakatangaze. Leo mmewafunga mikono, TANAPA hawaendi kutangaza utalii. Niwashukuru kwa kazi waliyoifanya akina Ndugu Kijazi sasa hivi shilingi bilioni 237 zinaingia ndani ya TANAPA na inasaidia kwa ajili ya Watanzania lakini ndani ya uwindaji hakuna kitu. Tusishabikie vitu vingine unaona kabisa vinaukakasi ndani yake, mtanisamehe kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia corridor za wanyama. Tanzania kulikuwa na mipaka ya wanyama. Rukwa – Rukwati wanyama wanatoka Zambia wanaingia mpaka Rukwa wanakwenda mpaka Kibaoni. Wanyama wanatoka Nyasa wanaingia Selou wanakwenda mpaka Kaskazini lakini njia zile zote zimevurugwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nailaumu Serikali kwa sababu waliuachia uozo huu. Wananchi wamevamia corridors za wanyama, mnyama atakwenda wapi? Mnyama hana mtu wa kumtetea lazima wapatikane watu wa kuwatetea kama Riziki Said Lulida. Mimi ni mtetezi wa wanyama kwa kujua kuwa tulikua nao, mimi nimezaliwa Selou, tumezaliwa na tembo, walikuwa wanapita katika njia zao, njia mmeziharibu mnategemea nini? Mnategemea wale wanyama watakwenda wapi? Hata tukisema tutakula, je, utalii au vizazi vyetu vitakuwa na uwezo wa kuona wanyama hawa baada ya miaka 100? Tunataka tuwe na sustainable tourism ili watoto wetu katika miaka 100 waje waone kizazi cha tembo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika research iliyofanyika hivi karibuni wamesema kwamba kama Tanzania hatutasimamia wanyama baada ya miaka 100 hakutakuwa na tembo, ile the big five yote itapotea. Ni kweli leo unakwenda Serengeti unamtafuta simba na chui, ni kwa sababu ya binadamu. Binadamu wanaingia ndani ya mbuga wanatafuta vimolo, wanachinja wanyama ilhali wakijua wanyama wale wale watalii wanatoka nchi mbalimbali kuja kuangalia utalii wetu na kwa kweli tumeuboresha umefikia katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema tunatafuta kuongeza kipato. Leo TANAPA wanafanya utalii wa msimu tu, ikifika kipindi cha masika daraja zote zimejaa maji. Ningeomba Serikali itengeneze daraja au iwape mkopo watengeneze Madaraja ya Kilawira, Kogatende, Grumeti na mengineyo ili angalau watalii wawe wanaweza kuja Tanzania mwaka mzima maana kuja kwa msimu tunapoteza tozo nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru watu wa hoteli (TATO), tulileta kelele sana kwa sababu walikuwa hawataki kulipa concession fee. Nimepata taarifa kwamba sasa hivi wanalipa concession fees. Penye haki semeni haki na penye uozo lazima tuwaambie pana uozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaizungumzia Selou. Selou ina ukubwa wa kilomita za mraba 153,000, Ruaha ina ukubwa wa kilomita za mraba 44,000, Serengeti ina ukubwa wa kilomita za mraba 12,500. Zimeletwa hela za World Bank, narudia tena, nilizungumzia katika hoja ya Waziri Mkuu, zililetwa hela na World Bank kwa ajili ya Selou. Unapozungumzia Selou unaizungumzia Lindi, Mtwara na Ruvuma. Zile hela zimetolewa zimepelekwa upande wa pili, barabara ya kutoka Kilwa kwenda Liwale haipo, huyo mtalii atapitia wapi? Wanasema tunataka kuendeleza utalii Kusini ....
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali Wizara ya Maji na Umwagiliaji 2018/2019
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote ninakushukuru na mimi kwa kunipatia nafasi hii kuchangia hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Spika, sina matatizo na Waziri, Naibu Waziri wala Katibu Mkuu hawa ni wageni, mimi kila nikizungumza nazungumza tuwe wazalendo kwa nchi na Taifa letu. Tukiangalia pesa na mikopo mbalimbali inayotumika kwa ajili ya maji, tukatathmini na maji yaliyopatikana kwa kweli ni mtihani mzito sana kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia kwanza Manispaa ya Lindi na Mradi wa Maji wa Lindi mpaka Mheshimiwa Rais alipata hasira kutaka kumtia ndani yule consultant. Jambo la kushangaza taarifa atakayoambiwa Waziri ataambiwa Lindi kuna maji wakati Lindi hakuna maji. Ule mradi unatia huruma na huzuni kwa nchi hii, zimetumika pesa za mkopo lakini akaunti imefunguliwa India siyo Tanzania. Consultant anakaa India, anatoka India kwa mwezi kuja kuangalia mradi Lindi na anafikia katika mahoteli makubwa anatumia gharama kubwa lakini gharama zile zipo ndani ya huu mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukifikiria huu ni mkopo, wao wanatumia gharama nyingi sana kuliko hata uwekezaji wenyewe wa maji, sasa hasara hii nani mnataka abebe? Hii ndiyo miradi yote ya maji unayiona Tanzania imefikishwa hapo, kuiingiza nchi katika dhahama wakati wao ndiyo wanafaidika hapa tunaendelea kubeba mikopo mikubwa ambayo haina faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa Mjumbe wa Bodi ya Maji Lindi, mradi wa kutandika mabomba alipewa Ms Jandu, amechukua mara ya kwanza shilingi bilioni saba kutandika mabomba ya maji yakapasuka, akaomba tena bilioni sita ikawa shilingi bilioni 13. Leo ninachokuambia Lindi ukifungua maji yale mabomba yanapasuka, Serikali inaingia tena mzigo wa pili kwa kutengeneza mabomba na siyo kumuadhibu yule mkandarasi. Jamani tunakwenda wapi, huyu mkandarasi yupo na amepewa tena ndiyo miradi miwili wa Chalinze na wa Lindi, miradi hii yote miwili haifanyi kazi, wenyewe wanakaa India, kila kitu India na akaunti India. Hii ndiyo mikataba mibovu ya maji! Haimuhusu Waziri Kamwelwe wao wanaohusika ndiyo wataijua kwa nini wanatuingiza katika mikataba ambayo nchi inapata frustration ya kutosha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiiangalia miradi hii ya mikopo ya World Bank Tanzania nzima utaona ni kafara, kafara hii itawaangukia hawa ambao mwanzo wala mwisho. Tulipewa semina ya jinsi Watanzania tunavyopata tatizo katika masuala ya miradi. Tupo vizuri kuandika feasibility study, kufanya strategic plan, action plan na commitment lakini tupo poor katika management. Ameizungumza Mheshimiwa Ridhiwani kwa kweli usimamizi mbovu hata kama tutawaletea shilingi bilioni 500 bado maji hayatapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kitabu hiki nimeona cha Wizara ya Maji wanasema tuna upungufu wa wataalam kwa vile wale watalaam wa zamani wamestaafu, sasa hata kama unapeleka pesa hauna wataalam kuna nini tena hapo? Ina maana wewe unachukua pesa unapeleka kwa watu ambao siyo wataalam, matokeo yake zile hela zitafujwa na wananchi watakuwa hawapati maji. Tathmini yake ni kuwa hizi hela mnazozipeleka kwa vile hakuna wataalam, hakuna maji, aibu. Tufike mahali tujiulize tumekwama wapi, tumenasa wapi. Suala la kusema tunaomba pesa sikatai ombeni pesa, lakini je hizo pesa zitafanya kazi iliyoandaliwa? Hamna wataalam mnazungumza na kama hamna wataalam kila siku mlikuwa wapi msiseme suala la wataalam, mnafika mahali sasa hivi mnapigana na hela lakini hela ile mkiitoa hamna mtaalam, yale maji yatapatikana wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulipata miradi ya World Bank katika vijiji pamoja na Mradi wa Sabodo, jambo la kusikitisha nenda Mchinga hakuna maji, ina maana surveyor na mchimbaji ni watu wawili tofauti, hawana ushirikiano na matokeo yake maji yamekwenda kila walipochimba maji Mvuleni, Mchinga, Kilangala na Chikonje hakuna maji. Hivyo, tena wanatafuta pesa zingine kupeleka kwa ajili ya maji wakati hela zilishapelekwa, hii ni double standard inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inanisikitisha kujiuliza suala la maji unasema unataka kumkomboa mwanamke, hata wanaume wanaweza kujitika maji maana haiwezekani kuleta kuwa lazima maji ajitwike mwanamke, hapana vilevile wanaume wanayo haki ya kuchota maji lakini suala la kujitwika maji na kukomboa maji ni lazima liwe la kila Mtanzania lakini uwepo uzalendo kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la mazingira na tabianchi, nimehudhuria mikutano ya mazingira na tabianchi. Kwa vile Serikali haioni umuhimu hakuna wawakilishi wanaokwenda kuhudhuria mikutano ya mazingira na tabianchi (climate change). Nimekwenda mwaka jana na mwaka juzi hakuna Waziri aliyewakilisha, nchi nzima haina uwakilishi sasa utapate taarifa ya climate change ili angalau muweze kuangalia nini tufanye, haya maporomoko ya maji yanasabishwa na nini ina maana hamtaki kujifunza vitu ambavyo baadae vitakuja kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unakuta kuna mradi unatakiwa shilingi bilioni 500, nakubali lakini kuna kitu kinaingia ndani yake kwanza consultant na ma-expatriate wanatoka India wanaingia ndani ya huo mradi, matokeo yake wao peke yake watatumia karibu shilingi bilioni 100, sasa hata kama utaniambia nalipa ile riba kwa miaka 20 lile deni ina maana kila mwaka mimi nikilipa shilingi bilioni 25 mwakani ita- subsidize itabakia pale pale, ule mradi utachukua hata miaka 50 Serikali hii haiwezi kulipa lile deni na itakuwa ni madeni ya kudumu kila siku tunaingia katika madeni ambayo hayalipiki.

Mheshimiwa Spika, kama mdau naomba andaa Tume Maalum ikaangalie kuna nini kwenye maji, mikataba yao na usimamizi wao uje utupe ripoti hapa tuweze kuichangia tuweze kuijadili. Masuala ya kumuingiza mbuzi ndani ya gunia ukaniletea mbuzi sokoni mimi silielewi. Mara nyingi tunafanya miradi wanasema mikataba sikuoneshi, kama hata Kamati ya Bunge ya Sheria Ndogo haioni mikataba hii inasema nini, mnatuambia nini hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mikataba imefichwa na kama imefichwa kinachoendelea ni nini, ni kuhakikisha nchi inaingia katika dhiki kubwa ya maji lakini hela zinaliwa na wageni.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hapo nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nakushukuru nami kunipatia hii nafasi ya kuchangia hoja iliyokuwa mezani. Kwanza nakupongeza kwa kazi kubwa uliyoifanya kwa kuunda Tume ya Bunge kuangalia udhaifu uliojitokeza katika makinikia pamoja na uvuvi. Hii imeleta faraja kubwa katika Bunge letu, kuwa sasa hivi Bunge linafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, mwanzo lilikuwa Bunge ambalo unaona kabisa lipo lipo lakini naona sasa hivi umeliamsha dude ndani ya Bunge na Bunge liko vizuri. Nakuomba tena, tunataka Bunge Live ili hayo unayoyaunda watu wayasikie kule mtaani. Wananchi, wapiga kura wanataka kusikia nini unazungumza, Wabunge wako wanafanya nini? Hii kazi itasaidia kuweza kuleta uelewa kwa wale watu, watakuwa wanajua kinachoendelea ndani ya Bunge. Hoja za Wabunge wao zinazungumzia nini? Tukikaa humu ndani wananchi hawaoni hayo unayoyafanya. Kwa hiyo, ningeshukuru sana na hilo nalo ungeliamsha ingeleta tija zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona kuna hoja nzito ya wafanyabiashara, wakulima dhidi ya kuwa na mahusiano mabaya na mabenki. Benki zimeamua kuwakandamiza wafanyabiashara hasa wakulima. Tumeona katika miaka miwili wakulima wako katika hali ngumu sana, wamelima mazao, lakini baada ya kulima mazao Serikali imewasimamishia maendeleo yao kwa kutokununua mazao yao. Matokeo yake benki hazikai chini kuangalia nini tatizo la hawa wakulima? Matokeo yake sasa hivi kila benki inataka kuuza mali za wakulima, mali za wafanyabiashara. Nafikiri Mheshimiwa Waziri akae chini na watu wa benki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Benki Kuu imepunguza riba kubwa sana kwa benki nyingine, nafikiri ni kama 9%, lakini benki hizo badala na wao kupunguza riba, wameongeza riba imekuwa kubwa sana. Imekuwa kubwa kiasi kwamba hakuna mfanyabisahara wa kawaida ambaye anaweza kukidhi haja. Ukiweka pesa wanaweka percent, ukitoa pesa wanaweka percent na ndani yake kuna udhaifu mkubwa. Nafikiri hata na maeneo haya ya benki yaangaliwe kuna nini? Kama Benki Kuu imepunguza riba, kwa nini bado wao wanaongezea mzigo mkubwa kwa wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali hii inakatisha tamaa kwa wakulima. Nataka nikupe mfano, nachukua mfano wa wakulima wako wa Kibaigwa. Pale palikuwa na wafanyabiashara wakubwa wa mazao, miaka mitatu wamekutana na crisis za mvua na pametokea mafuriko makubwa, wao bado wanaendelea na interest, lakini hawaangalii kuwa je, wenzao ambao wamekutana na mafuriko ambayo siyo wao, ni mipango ya Mwenyezi Mungu, wangekaa chini wakapunguza riba ile ili na wao waweze kufanya biashara. Matokeo yake wanawakandamiza na kutaka kuuza mali zao bila kuangalia nini tatizo.

Mheshimiwa Spika, Kenya, Waziri wa Fedha na watu wa benki wamesimama na wanafanya biashara. Nami nina imani kuwa Mheshimiwa Waziri ananisikia, atasimama na benki na kuangalia wafanyabiashara wakubwa wanaathirika vipi na mikopo ya benki ili kuweza kuisaidia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia TRA. Ukiona mahali ngoma inachezwa sana, basi haikawii kuharibika. TRA walileta EFD machine. Kuna siku nilifika katika petrol station karibu mara mbili, nikifika wananiambia mashine haifanyi kazi. Nikauliza kwa nini haifanyi kazi? Hela zinaendelea kuchukuliwa, lakini zile hela ambazo zinatakiwa ziingie katika Serikali haziingii. Nataka nijue idara ya ICT ya TRA inafanya kazi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama mpaka Mbunge amekuja kuliona hili suala humu ndani, baada ya siku ya pili tumeona mashine zinafanya kazi, hii ni hujuma. Hujuma kama hamuisimamii itakuwa ni hujuma kubwa sana. Kwa vile ICT Department ndiyo inaweza kuingiza data ndani ya program ya Serikali na kuingizia pato Serikali, lakini kama ICT Department ikicheza na ma-hackers kwa kufunga hizi EFD Machines hizi pesa zote badala ya kuingia katika Mfuko wa Serikali zitaingia katika mifuko ya watu wengine ambao sisi hatuwajui. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nijiulize swali, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kumaliza ku-wind up aniambie Department yake ya ICT iko makini? Huwa ni network, maana katika ICT inabidi ianzie TRA, iende mpaka katika mabenki, iende mpaka TCRA kuona je, humo ndani yake kuna nini ili angalau huu uovu, utasema Serikali haipokei mapato, kumbe mapato yanaingia kwa watu binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia suala la miradi mbalimbali ambayo imesimama kwa muda mrefu. Nataka nitoe mfano wa LNG (Liquefied Natural Gas) ambao uko Lindi. Tulitegemea mradi ule ungekuwa tayari umeshaanza kazi, lakini pamesuasua kwa muda mrefu, hatuambiwi mpaka leo ule mradi umesimama wapi? Huu ni mwaka wa tano wananchi wamechukuliwa maeneo yao hawajalipwa, lakini kinachoendelea hakijulikani.

Mheshimiwa Spika, hii inawapa mwanya wawekezaji kuchukua ile miradi kuipeleka Mozambique. Sasa hivi kila mradi ambao tunaukataa Tanzania, wenzetu Mozambique wanauchukua, matokeo yake badala ya kwenda mbele itakuwa sisi tumesimama na miradi yetu tukiwa na urasimu ambao mimi sijajua, lakini naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujibu aniambie.

Mheshimiwa Spika, kuna kitengo ambacho ni Taasisi ya CAG ya Ukaguzi. Kwa kweli hapa pana mtihani mzito sana. Kuna maeneo ambayo Serikali imeyaachia yasikaguliwe. Kwa nini? Kama Jeshi linakaguliwa na Bunge linakaguliwa, maeneo hayo ndiyo mianya mikubwa ya kupoteza hela ambazo sisi hatuzijui.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano. Wafanyakazi wote wa Serikali mishahara yao inapitia NMB. Madaktari mishahara yao inapitia NMB na taasisi zote za Serikali zinapitia NMB, lakini hapakaguliwi. Sasa hivi nataka kufikia mwisho mpaka binadamu yule au biashara yao imekufa unakwenda kufukua makaburi. Tuache biashara ya kufukua makaburi. Kama ni sheria, walete Bungeni, Bunge lipitie sheria, wakaguliwe NMB, NBC na taasisi zote ambazo inabidi zikaguliwe. Kama hawakagui ndiyo mianya inapita ya pesa kwenda nje. Kama hawaiangalii mianya hii, leo kama taaisisi kubwa, mikopo yote ya Serikali iwe ya wanafunzi, inapitia NMB, halafu wanasema hawaikagui, wanalionaje hili neno? Ni hatari kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni lazima CAG awe na meno. Sheria ya CAG iletwe irekebishwe, apate fedha za kutosha ili awe na uwezo wa kukagua. Ama la, CAG anakagua chini ya 40%, ina maana maeneo mengi anashindwa kukagua. Kama anashindwa kukagua, ni vipi wataweza kujua athari ambazo zinapatikana katika maeneo mbalimbali? Leo hii unamwona CAG anashindwa kukagua maeneo mengine. Hakuna haja ya kufichaficha, tuseme aah, hapa TAKUKURU tusikague.

Mheshimiwa Spika, kwa nini TAKUKURU isikaguliwe? Pesa zinazokwenda pale ni za Watanzania. Matumizi ya pale ni ya Watanzania. Kama watu hawa hawakaguliwi, ndiyo mianya hiyo, maana watu wanatumia pesa bila kukaguliwa. Maana Jeshi wanakagua, ndiyo ambapo nilitegemea ni sehemu nyeti sana, lakini anasema maeneo mengine hatukagui. Hiki ni kigugumizi ambacho hakina maana, naomba Mheshimiwa Waziri atakapoingia katiak ku-wind- up anipe majibu kwa nini maeneo mengine yameachwa yasikaguliwe, tunaachia watu tu wanatumia wanavyotaka wao, wanakuwa na viburi vya kutosha? Hivyo naiomba Serikali iifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia suala la barabara. Leo hii Mikoa ya Lindi na Mtwara ndiyo kwenye uchumi. Tunaona uchumi wa Mkoa wa Lindi kwa ajili ya korosho imekuwa ni green gold kulinganisha hata na madini mengine, lakini hatuna barabara. Tumekuwa maskini watu wa Mkoa wa Lindi, hapapitiki leo kwenda Liwale, Liwale ina Selous, lakini hakuna barabara, Liwale ina korosho, hakuna maendeleo ya barabara, Nachingwea hakuna barabara, Kilwa hakuna barabara. Sasa wanapelekaje uchumi bila kupeleka na barabara? Uchumi utakwenda sambamba na miundombinu. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri atuambie, bajeti iliyopelekwa katika maeneo yale yanayozalisha, Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma inakwendaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye amenijaalia kuweza kuwa hapa na kuweza kuchangia katika hoja iliyopo hapo mezani. Vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu aliteremsha vitabu vinne na aliwateremshia Manabii mbalimbali ikiwemo Injili alimteremshia Nabii Issa (Alayh- Salaam); Taurati kwa Nabii Mussa; Zaburi kwa Nabii Daud na Quran kwa Nabii Muhammad (Swalla-Allah Alayh Wasalaam).

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia na madhumuni ya kuteremsha vitabu hivi ni kuwaweka binadamu katika mfumo wa kujua kuna Mwenyezi Mungu na kumwabudu Mwenyezi Mungu katika matendo yaliyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vitabu hivyo vyote hakuna mahali palipozungumzia suala la ushoga. Ushoga ni dhambi ambayo haitakiwi na inatakiwa ikemewe, sio mfumo wa kiafrika ni mifumo ya watu wa nje, wao waendelee na mifumo wao na watuachie na utamaduni wetu wa kiafrika wa kumuabudu Mungu aliye sahihi katika vitabu vyake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hapo ninakwenda katika hoja iliyopo mezani. Mipango iendane na maeneo ambayo sasa hivi yalikuwa nyuma kwa muda mrefu. Mkoa wa Lindi, Mtwara, Ruvuma, Rukwa, Kigoma na Singida hii ni mikoa ilikuwa nyuma na Serikali inahitajika isimame kutoa kipaumbele na kuwahurumia wananchi wa maeneo hayo ni na wao waendane na wenzao. Nitazungumzia Mtwara Corridor na baadhi ya maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usinione pengine napenda sana kuangalia Mikoa ya Lindi na Mtwara, ndiyo mikoa ambayo iko nyuma, hakuna cha kubishana katika hilo. Tuliletewa Mradi wa LNG (Liquefied Natural Gas), ule mradi umenyamaza, upo kimya, hatujui kinachoendelea ni kizunguzungu. Wananchi wa eneo la Likong’o wamechukuliwa maeneo yao huu ni mwaka karibu wa nne au wa tano hawaruhusiwi kulima wala kufanya maendeleo ya namna yoyote, hawajalipwa fidia zao na hali ngumu ya uchumi kama hivi tunategemea watu kama wale wanafanya nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri mwenye dhamana atuambie mradi mkubwa kama ule umefikia wapi hata kwa kutoa semina kwa Wabunge, Wabunge wawe na uelewa, lakini wale wananchi ambao wananyanyasika na ardhi zao, hawajui wanalima nini, wanakula nini, Serikali imetumia kitu gani cha kuwasaidia wale watu. Wamejipanga vipi kuwainua watu wale ambao ni maskini wanategemea mikorosho na kilimo chao wapate chakula, sasa hivi hawana chakula. Naomba Serikali yenye dhamana ikawahurumie wale watu na iwatengenezee mazingira bora kwa kila Mtanzania inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuja katika suala la mazao mchanganyiko kuna korosho, pamba, alizeti, katani, dengu, maharage na kadhalika. Wananchi wamekwama na mazao yao, hawajui wafanye nini. Mbaazi za mwaka jana hazikuuzwa zimekaa majumbani na nyingine zimeachwa shambani mpaka zimeharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe angalau ushauri; Rwanda wenzetu wamejiingiza katika mfumo wa kibiashara unaitwa African Improvement Food. Hiyo maana yake wamejiunga na taasisi mbalimbali za nje wanatengeneza mifumo ya mazao yao kupeleka direct nje bila kupitia kwa wababaishaji wa katikati ambao wametunzungusha kwa muda mrefu. Leo karanga za Dodoma, Singida na Shinyanga zinapelekwa Rwanda na kahawa ya Bukoba inapelekwa Uganda. Sasa tujiulize kwa nini wenzetu wameweza sisi tumeshindwa wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na taasisi moja Board of External Trade sielewi imefia wapi, ina maana wale wange-link na mashirika mbalimbali ya nje ya kibiashara kama soko la European Union tungekuwa sasa hivi tusingekaa tunababaishana na watu ambao wameshakuwa wababaishaji tumewatajirisha sasa hivi wamekuwa wanatudhalilisha katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ubabaishaji wamezoea kutuona wananchi wa Tanzania tukiendelea kuwa maskini wao waendelee kuwa matajiri na hawapo tayari kushirikiana na sisi angalau kututoa katika umaskini. Tanzania ya kuweza kusaidia viwanda na maendeleo ya kilimo inawezekana, tujipange tunaweza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni champion na hoja mara nyingi itakuwa haieleweki lakini kutakuwa na siku watu wataielewa. Nina hoja kubwa ya Selous, nina hoja kubwa ya mjusi tunakimbizana na mama ntilie. Pato la mjusi nani analisimamia? Nataka nitoe onyo au niisaidie Serikali kwanza Lindi Vijijini iitwe Tendeguru District, maana yake ukisoma suala la Tendeguru wanasema it’s a loss science, it’s not a loss science, it’s a life science. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wanavyosema Tendeguru haijulikani duniani wakati mimi Riziki nilikuwa Tendeguru juzi na watakapokuja wao wakienda kuvumbua pale wataonekana sisi tumeiacha Tendeguru haionekani. Naomba kila Mtanzania ajifunze kukimbia na maendeleo ya Tanzania. Mapato yale kuyaachia vijiji vile wakiwa hawana shule, maji na barabara; revenue ambayo inapatikana kule tuje na sisi tupate mrabaha, tatizo lipo wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku nalizungumza tatizo lipo wapi? Mjusi yule toka mwaka 1903 yuko Tristan Ujerumani wanafanya exhibition, wanapata mapato, hivi jamani Serikali hii mnashindwa hata kujua Lindi inapata nini au tozo yake ni nini? Mimi nakuwa hapa kila siku nayumba napiga kelele hamnielewi ninalolizungumza, lakini nina imani kutatokea watu wachache watakaoniunga mkono na kulielewa hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia Selous; Selous ni ya pili katika dunia kwa ukubwa wake. Selous ni eneo ambalo ni shamba la bibi linachezewa, watu wanachimba madini, wanamaliza wanyama na matokeo yake pato la utalii wa Tanzania litapatikana wapi. Kuna corridor ya Tembo kutoka Selous kwenda Niyasa na Niyasa – Selous. Kuna corridor ya Tembo kutoka Rukwa Rukwati kwenda mpaka Katavi – Zambia, hizi corridor zote hazijakuwa promoted. Tunahitaji kufanya promotion ya kutosha na tutoe hela ya kutosha utalii wa Tanzania badala ya kutegemea asilimia 17.2 naomba sasa hivi kwa pamoja tujipange.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu ambao tupo katika Kamati moja ya Kupambana na Ujangili na Kuendeleza Conservation twende kwa pamoja tupambane kwa hili mpaka tujue Selous inapata pato la aina gani na matumizi yake yanakwendaje ili nchi nayo ipate uchumi bora badala ya kukimbizana na mama ntilie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja upande wa barabara. Ili tuendelee tunahitaji uchumi bora ambao utapatikana katika mawasiliano na ikiwemo barabara. Nahuzunika sana, juzi wamekwenda kupiga kelele Liwale wamepata kiti Liwale lakini Liwale iko kisiwani. Ina maana wanawapenda watu wa Liwale wawapigie kura lakini Liwale iendelee kuwa kisiwa, zikianza mvua za mwezi wa 11 hakuna hata Mbunge wa Liwale kwenda Liwale, mimi sielewi. Kwa nini wanawafanya watu wa Liwale wawe kisiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Dar es Salaam ukifika Nangurukuru kwenda Liwale unazunguka mpaka Nachingwea, ni miezi mitatu tu ndipo unakwenda Liwale. Wanalima korosho, ufuta na mbaazi hali yao ni duni kwa vile hawana barabara. Naomba Mwenyezi Mungu alijaalie Bunge hili na wanaonisikia hao wenye kuweka hizo hela na mafungu waisaidie Liwale, Nachingwea na maeneo mengine ili uchumi wa Tanzania uweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sina mengine, nawashukuru sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru nami kwa kunipatia dakika chache ili nichangie katika hoja iliyoko mezani. Mwenyezi Mungu aliumba binadamu, aliumba ardhi, akaumba binadamu, wanyama, mito, bahari, wote hawa walikuwa wanategemeana. Nimefurahi kusikia baadhi ya mashamba yamerudishwa Serikalini ili kuwasaidia wananchi waendeleze kilimo, hii maaana yake nini? Niliwahi kuzungumza suala la baadhi ya mashamba ikiwepo mojawapo shamba la Kikwetu lilikaa kwa muda zaidi ya miaka 40 halilimwi, watu wanachukua mikopo benki, mashamba yale wakipewa wananchi, nina imani kuwa tutasaidia wananchi kupata ardhi na kuweza kulima.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mashamba yalikuwepo Mtwara Kabisela, mashamba yale yalikuwa yamepigwa uzio, huruhusiwi kuingia, matokeo yake kinachoendelea ndani hujui. Huu ni unyonge ndani ya nchi yako, watu wana- monopolize ardhi lakini haitumiki.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia suala la uhifadhi Tanzania; Tanzania kuliwa na GN ambazo zilishawekwa kwa ajili ya uhifadhi kwa asilimia 25, lakini GN hizo zipo katika makaratasi, ukienda kwenye uhalisia tayari wananchi wameshavamia maeneo yale. Narudia tena naomba busara itumike na busara itumike kwa nini? Mle ndani ya zile hifadhi kuna wanyama, kuna korido za wanyama ambao wanatoka katika njia zao wanaingia ndani ya mbuga za wanyama. Kwa mfano, Mheshimiwa Spika mwaka 2005 alikuwa ni mjumbe mwenzangu katika Kamati ya Maliasili na Utalii, tulikwenda Ihefu kuwatoa wafugaji ambao walishaharibu mazingira na nchi ilikuwa gizani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tunataka kuruhusu bila kufanya utafiti, hili zoezi litakuwa gumu na litaiingiza nchi katika mazingira magumu tena. Wanyama hawa waliandaliwa na Mwenyezi Mungu kupita katika korido zao, leo tumeona Ivory Coast hakuna wanyama sasa hivi, tunaona Burundi hawana wanyama, tunaona Rwanda hakuna wanyama, sasa Tanzania tumevimbiwa na wanyama wachache tunawaona hawa, lakini ni uchumi bora ambao utaifanya nchi iweze kupaa kama tutaweza kuweka mazingira bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanyama tembo, simba, chui anatoka Niassa Mozambique, anavuka Mto Ruvuma anafika Mbarang’andu wananchi wameshavamia eneo, tembo wale wanauawa, hivyo mpaka kufika Selous karibu nusu ya tembo hawarudi tena Mozambique. Tembo anatoka Namtumbo anataka kuvuka kwenda Matambwe kwenda Mikumi tayari watu wanalipa miwa, mnyama hana mahali pa kwenda. Tembo anaingia Mikumi anataka kwenda Mkungunero tayari ameshazuiwa katika. Leo wanapotaka kutoa maamuzi ya kukurupuka, naomba tena tukae chini tuliangalie suala la wanyamapori ama la, nchi itaingia katika hali ngumu na wanyama watatoweka, utalii tunaojivuna nao utapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania tunajuana kwa makabila, kuna makabila wanapenda uhifadhi kama Mmasai, Mmasai hali nyamapori na hakati misitu. Kuna Wamakonde wanatunza misitu ndiyo maana misitu hiyo ilihifadhiwa mpaka leo, leo wafugaji wamekwenda Kusini, Lindi sasa hivi ni jangwa. Tunaona mikoa mingine imeshakuwa jangwa, je, hili zoezi litatusaidia au litatuwekea hali ngumu, nchi ni jangwa, ukiingia Dodoma yote ni jangwa, Singida jangwa, ukiingia Mkoa wa Arusha yote, Monduli jangwa, Shinyanga yote jangwa, tutafakari kabla hatujatoa maamuzi ambayo yataifanya nchi i-paralyze, kurudisha tena hii hali itakuwa ngumu.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya wafugaji au makabila, kula nyama pori ni kama kazi yao, kama mtu wa Serengeti kazi yake anakimbizana kuingia ndani ya mbuga kula kimoro. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru sana na niwashukuru Spika, Naibu Spika, Katibu wa Bunge, wafanyakazi wa Bunge na Wabunge wenzangu kwa kunisaidia na kunitoa huzuni kipindi kigumu cha kupata msiba wa mtoto wangu ambaye alifariki. Nawe Naibu Spika ulikuwa mmoja wapo wa waliokuwepo mpaka tunasafirisha mwili wa marehemu kupeleka Dar es Salaam na tumezika, nashukuru Alhamdulillah. Mwenyezi Mungu awawezeshe na awalinde na Mwenyezi Mungu wote anasema Inna lillah wainnailayhi rajiuun na kila nafsi itaonja umauti (kullu nafsin dhaikatul–maut).

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Waislamu wote Tanzania na wasiokuwa Waislam kwa mwezi Mtukufu wa Ramadhan, nawatakia Ramadhan Kareem na Mwenyezi Mungu atujaalie katika Mwezi Mtukufu huu ailinde nchi yetu iingie katika amani, tusidhoofishwe na mabeberu ambao wanataka kutugawanisha na kutuweka katika mazingira magumu. Tanzania yenye amani inawezekana. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, nitazungumzia suala la barabara, lakini hasa nataka nizungumze kwa dhati ya moyo wangu kuwa, kuna ubaguzi mkubwa unatendeka kwa kupitia Mawaziri wetu katika ugawaji wa barabara. Barabara haitakiwi kuonekana upande mmoja unapewa priority na upande mwingine unaachwa ukiendelea kulalamika kila mwaka. Hii haileti ufanisi na umoja tuliokuwa nao katika Tanzania hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie Mkoa wa Lindi katika mikoa nane ya ukoloni, tulikuwa katika mojawapo ya province nane za Tanzania, lakini leo kwenda Liwale, Liwale ni Wilaya ya zamani sana, inakuwa kama wako kisiwani. Watu wa Liwale wako Guantanamo. Leo mvua inanyesha inawachukua miezi mitatu mtu wa Liwale aweze kuja Dar es Salaam, akipata ugonjwa Liwale hawezi hata kwenda Lindi, jamani tufike mahali tusema basi tufunge ukurasa. tumelalamika barabara ya Liwale toka Waziri Mkuu wa Jimbo la Liwale alikuwa Rashid Mfaume Kawawa, wanamuenzi vipi Kawawa katika Jimbo lake? Wanachofanya kipindi cha uchaguzi kutumia nguvu kubwa kutaka Jimbo, lakini je, wananchi wa Liwale wanawafanyia nini? Kwenda Liwale ni kama adhabu na mfanyakazi wa Tanzania akitaka kuadhibiwa mpeleke Liwale. Mfanyakazi wakijiona hawamtaki wampeleke Liwale kwa maana Liwale ni Guantanamo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimezungumza kwa miaka, nimepewa ahadi na Mawaziri kwa miaka, Mheshimiwa Mramba mpaka akasema mama mwaka huu ni wa mwisho nitakupelekea lami Liwale. Kwa masikitiko nataka niseme kitu kimoja kwamba, Bunge tutengue Kanuni ya kushika Msahafu au Biblia kwa kusema uongo humu ndani. Watu wanashika Biblia mwaka huu barabara itapatikana lisemwalo silo! Kwa nini tunashika Quran, kwa nini tunashika Biblia ikatuleta katika uongo, ina maana inatuingiza katika uongo na laana katika Bunge. Tutengue Kanuni, tutumie Katiba badala ya kutumia Quran maana Quran haitaki kusema uongo wala Biblia haitaki kusema uongo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amezunguka Mtwara pamoja na mama Janeth, amesema kazi aliyoiona kwa barabara za kule kweli amehakikisha kwamba barabara ni mbovu, lakini kuna maeneo yanapata upendeleo, upendeleo kila mwaka, hii mpaka lini? Leo kwenda Liwale unaona Liwale mpaka Nachingwea barabara kubwa kiuchumi katika mikoa inayozalisha korosho, ni mikoa miwili ambayo na wa tatu ni Ruvuma. Wa kwanza ni Mtwara, wa pili Lindi na wa tatu ni Ruvuma. Asilimia 80 ya korosho ambayo ni uchumi mkubwa katika nchi hii inatoka sehemu hizo, lakini hakuna barabara. Wanalalamika kuhusu kangomba, mtu yuko kijijini, anaitoaje korosho yake kijijini kupeleka katika magulio wakati hakuna barabara, sasa wale walanguzi wanakwenda kuchukua kule kwa ku-risk na magari yao kutoka kule mpaka kufika mjini, leo wanawakamata watu kwa ajili ya kangomba, lakini je, wamewawekea barabara? Huwezi kumkata mtu bila kumwekea alternative, kunatakiwa kuwepo na alternative, barabara ziwepo vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo mikoa ambayo ina uchumi mkubwa sasa hivi tumeona LNG inaenda sasa hivi, miradi inakamilika kutaka kujenga liquefied national gas industrial area ambayo itawekwa Lindi, lakini hatuna airport! Ni kilometa 20 only kutoka airport kuja Kilikong’o, hakuna bajeti ya airport, je, hawa wafanyabiashara wakubwa wanaokuja kuwekeza katika mradi mkubwa wa matrilioni wataruka na ndege kutoka Mtwara. Mtwara mpaka Lindi wakati Lindi uwanja wa ndege kwa taarifa ya Bunge wa Lindi ni wa pili katika Afrika. Ndege ya kwanza ilikuwa inatoka London inatua Misri – Alexandria inakuja kutua Lindi inakwenda Afrika Kusini, tuko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanawafanyia nini wananchi wa Mkoa wa Lindi? Kwa nini wanatudhalilisha wananchi wa Lindi? Tumefanya nini katika nchi yetu? Keki hii hii ya korosho na vitu vingine wengine wanafaidika zaidi kuliko kuyaangalia maeneo ambayo yana uchumi na uchumi bora katika nchi hii yametupwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi, Mtwara na Ruvuma sasa hivi inabidi iwekewe EPZA yake ifanyiwe kazi kwa vile ndiyo mikoa ya kiuchumi, hakuna barabara. Utasikia barabara zinapeleka maeneo hata uchumi haupo na ubaguzi huu wa kupeleka fund nyingi katika maeneo mengine unauona kabisa. Tufike mahali bajeti isimame bila kuangalia pale paliposimama na maendeleo makubwa pasimame waende kwa maeneo ambayo watu ni maskini ili nao hawa wafaidike na sungura wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari ya Lindi ilikuwa ni bandari kubwa. Leo je, bidhaa zitaanza kupatikana kutokana na miradi ya LNG, bandari iko wapi? Bandari iko Lindi, ukienda uani huwezi kuona utafikiri kichaka fulani tu, watu hata kuweka bajeti hamna, bajeti za kibaguzi, halafu wanakuja kutumia nguvu kubwa wakati wa uchaguzi maana yake ni nini? Haiwezekani! Wamefikia mahali wanawafanya watu wanakwazika kujiuliza na inakuwa ndiyo mahali pa watu kwenda kupiga vijembe, ninyi maskini, mikoa imetupwa, lakini ni kweli mikoa imetupwa. Nenda leo Liwale kuna nini, nenda leo Milola kuna nini? Kutoka Lindi kwenda Milola hakuna barabara. Milola kwenda Nangaru na daraja limevunjika huu mwaka wa ngapi hakuna kinachosemekana. Nawaomba mpaka na Mawaziri kaangalieni mazingira, hakuna mtu anaye-take action nini maana yake? Basi tuamueni turudi Tanganyika yetu, tukakae na Tanganyika yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulifikia mahali tuliamua kuchanga kwa ajili ya kusaidia Lindi yetu tukasema haiwezekani, Lindi itachangiwa na Tanzania nzima, kuna nini Lindi? Barabara za Lindi ziko wapi? Nenda vijijini huko watu wanatembea kwa mguu, wanajitwika mitenga ndiyo maana hata wanakuwa wafupi kwa sababu kutwa mtu ana tenga kichwani. Hali hii ya umaskini wanayoipeleka Lindi inasababishwa na Serikali. Naomba barabara zikasimamiwe, nikitoka hapa nataka mguu kwa mguu na Waziri wa Ujenzi twende tukaangalie barabara Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefika mahali tuseme wazi kuwa kuna maeneo mengine imetosha tupeleke mikoa ambayo iko maskini na mikoa ile barabara ipatikane, maji yapatikane, afya ipatikane, sio kwingine watu wanaburudika wame-leisure sisi wengine kwetu tunahangaika, tunatembea kilometa nyingi kwa miguu, kwa nini na wakati nchi hii ni yetu wote? Uchumi ni wetu wote, korosho yetu na mapato yapatikanayo kutokana na korosho ni ya Tanzania nzima, lakini sisi wenyewe tumewekwa nyuma tumekuwa kama boga, unasuka mkeka mwenyewe unalala chini. Hii haiwezekani na haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, gesi sasa hivi naona tayari mikataba inapita maana yake naona ninapoona, lakini cha kujiuliza gesi ile maendeleo yake yako wapi, barabara zake za kupitisha vitu hivyo iko wapi? Inapita maporini humo hakuna kitu, hakuna barabara, mawasiliano yamekuwa magumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nasema ahsante imetosha. Tunataka Lindi yetu yenye barabara, Lindi yetu yenye afya, Lindi yetu yenye maji na hii inawezekana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuchangia katika hoja iliyoko mezani. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunijalia kupata nafasi hii. Nitaanza kuchangia katika suala la mazao mkakati ambayo unayaona hayamo ndani ya utekelezaji katika bajeti nzima ya mwaka huu. Zao la kwanza katika Tanzania ambalo linaingiza uchumi mkubwa ni zao la korosho. Hata hivyo, zao hili la korosho halimo kabisa kama ni zao ambalo linaweza kuchangia uchumi wa nchi wameliacha nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima analima, anasafisha shamba, anapulizia dawa, lakini unapofikia wakati wa kuuza anaanza kukwamishwa anaambiwa ana kangomba, sasa nini maana ya kangomba? Ni vitu ambavyo vinajitokeza kuwakwamisha wafanyabiashara wasiweze kufanya biashara ya tasnia ya korosho. Kwenda kununua mchele Mbarali sio kangomba, kwenda kununua mahindi Rukwa sio kangomba, kwenda kununua chochote sio kangomba, kangomba inaingia kwenye zao la korosho. Tujiulize swali, je, huyo mwananchi aliyekuwa kijijini maporini, barabara hakuna anaipelekaje korosho yake Liwale Mjini? Mwananchi aliyekuwa Namtumbo kijijini anapelekaje korosho yake Namtumbo Mjini wakati hakuna barabara? Sasa iweje watu wengine wanapewa nafasi ya kuleta mazao yao wakayauza huria lakini inapofika tasnia ya korosho tunaambiwa ni kangomba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wameshindwa kufanya biashara zao safari hii, wamekwamisha uchumi kwa ajili ya kangomba. Naiomba Serikali iliangalie neno la kangomba ilifute kabisa kwa vile kama wengine wanaweza kufanya biashara Tanzania nzima haina haja ya kuliweka neno la kangomba likawakwaza wananchi. Mwananchi amekaa Mpigamiti anataka kuja Liwale hana gari, hana usafiri, anapelekaje korosho yake. Naomba hili neno la kangomba lifutwe kabisa linaleta chuki na maudhi katika maeneo ya wakulima wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la korosho na mazao mengine mchanganyiko hayakutengenezea mfumo wa kibiashara ambao ungeweza kusaidia mazao yao yaweze kununuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Rwanda wametengeneza one stop center kwa ajili ya manunuzi ya biashara zao, wamejiingiza katika World Trade Center mbalimbali duniani, leo sisi tunategemea mazao yote tupeleke Kenya au Uganda au Rwanda, tujiulize wataalam wetu wanafanya kazi gani hapa Tanzania? Wanafanya nini kuhakikisha wana-promote mazao? Tanzania tuna mazao lakini huwezi kuuza mazao yako mpaka yapelekwe Rwanda, kwanza tujiulize tumezidiwa nini na Rwanda mpaka sisi tukashindwa kufanya vile? Pana upungufu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kakunda alikuwa mjumbe mwenzangu, namfahamu, ana uwezo mkubwa sana, pale unapoona kuna watendaji ambao huwezi kufanya nao kazi, bwana mhamishe au mtoe, sasa hivi tunataka Tanzania yenye uwezo, yenye uchumi na utekelezaji katika masuala ya biashara na viwanda. Hao ndio tunakwenda nao na unamwona Mheshimiwa Rais amesimama, ana uchungu lakini, je, unao watendaji wa kufanya nao kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja suala la balance of trade; leo Tanzania tunasema tunataka uchumi wa viwanda, watu wameanzisha viwanda, leo Kiwanda cha Dangote, tunaagizia katika miradi mikubwa ya Stiegler’s Gorge na miradi mikubwa ya SGR, wanaagiza cement Tanzania walikaa nao chini wakasema jamani ongeza viwango vyako ili angalau cement ya Dangote iende katika uchumi wa maendeleo tunayofanya sasa hivi. Matokeo yake dola imepanda, kila kitu sasa hivi na wahujumu wanapitia humo humo kuingiza cement kutoka nje, nondo kutoka nje, vifaa vyote vya ujenzi vinatoka nje, tutakwenda katika uchumi ambao hauna balance of trade. Tuna wafanyabiashara wanaoleta vinywaji, maji yanatoka China, juice zinatoka China, kila kitu kinatoka nje Bakhresa atafanya kazi gani, Udzungwa atafanya kazi gani, tumefikia mahali halafu wanapewa misamaha ya ushuru, wanapewa zero VAT, matokeo yake atakwendaje mfanyabiashara wa ndani, hivyo tunavokwenda ina maana tunapingana na mifumo na sheria ambazo zinawakwaza wafanyabiashara. Wafanyabiashara kila mmoja anafunga (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa vyandarua huko Arusha, chandarua kinatoka China zero kibovu, sasa huyu atauza chandarua bei gani A to Z ameshakuja zaidi ya mara tano anajiuliza zinaletwa chandarua mbovu na Tanzania bado tuna malaria, analeta chandarua ambacho kina dawa na kila kitu anaambiwa bwana, hawasikilizwi tu! Tumefika mahali tunajiuliza kweli tumetaka nchi hii tuiendeleze, mfumo tuliokuwa nao uko sahihi na uchumi wetu, tumejipanga kweli ama laa. Maana yake kujipanga at least 10 years mbele ili angalau tujue tunafanya moja, mbili, tatu, matokeo yake pale panaachwa hapa panashikwa, matokeo yake watu wamekaa desperate hawajui wanafanya nini kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imani yangu, tujipange maana yake nikiangalia nenda Temeke maduka yamefungwa, Kariakoo maduka yamefungwa, kila mahali maduka yamefungwa, leo Watanzania wanakwenda kununua bidhaa Uganda, bandari iko Dar es Salaam ukichukulia mzigo kutoka Dar es Salaam mpaka Uganda unalipwa lakini kwa nini anapata unafuu wa kwenda Rwanda, pana kitu kimesimama hapa. Sasa nataka niorodheshe katika vitu ambavyo vinaukwamisha uchumi wa biashara na viwanda kwanza TRA. TRA ni mwiba, mwiba, mwiba wa uchumi wa Tanzania, watendaji wabovu ambao wako ndani ya TRA wamejigubika wimbi la TRA wanaifanya nchi hii iyumbe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kusema ni wapi, isipokuwa waifumue TRA na waaangalie upungufu uko wapi, maana yake leo unafungua kampuni, hujaanza kazi wanakwambia tunakudai, watakusumbua na kesho wanakwambia tunakufungia. Mwenye kiwanda ana vurugu mara OSHA, pana regulatory bodies 47 atafanyaje kazi mtu kama huyu? Ina maana tumewakwaza wafanyabiashara wasitoke, matokeo yake tumebakia tumesimama, mbele hatuendi, nyuma hakutikisiki, mtihani kabisa mimi nauona huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inakuja ajira ndani ya viwanda, nilikuwa Kamati ya PIC, tukatembelea kiwanda cha EPZ cha kutengeneza jeans, unasema Tanzania tumeajiri watu 59,000 wameajiriwa kama vibarua, wanachukuliwa kila baada ya miezi mitatu. Baada ya pale anafukuzwa, inakuja benchi ya pili, hii huwezi kuita ajira. Ajira ambayo na analipwa mshahara mdogo kwa mwezi 100,000 na wanakimbia kuwa atalipwa haki zake za msingi. Sasa tunatakiwa tuangalie viwanda vinaendana na matatizo ya ajira, isiwe tunaleta viwanda lakini ajira tunawaletea watu wa nje na maeneo mengine kama unaenda unakuta wamejaa watu wa nje sio Watanzania. Tulisimamie suala la viwanda vya ndani na ajira ya Watanzania ili kuweza kuleta tija na Watanzania hao wajione wako katika nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejionea Kiwanda cha Dangote kikiajiri watu kutoka nje 120 mpaka wafagiaji, sasa tunajiuliza, watu wale wa Mtwara ambao tumesema tutapata opportunity ya kupata kazi na kupata ajira na kila kitu mpaka mfagiaji anatoka nje, tuna haja gani ya kuwa na Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeanzisha viwanda, tunasikia leo tumeleta matrekta, vijana hawa wadogo wanaomaliza darasa la saba ilibidi wapelekwe VETA wakasomee hata ufundi mchundo iwasaidie hata trekta likiharibika atakuwa anaweza kufanya kazi na ndio walivyotoka China, walivyotoka Thailand na nchi mbalimbali, lakini vijana wale wamekaa majumbani, wanacheza pull, wanakula madawa ya kulevya, matokeo yake mfumo wa kibiashara uliotengenezwa katika kipindi kifupi umefanya nchi imedhoofika na imedorora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nasema nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru na nimshukuru Mwenyezi Mungu anayenijalia afya njema na mimi kuwepo hapa na kuchangia hoja iliyokuwepo mezani. Kwanza napenda nitoe pole kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi ambao wamekutana na mafuriko makubwa ambayo hayajawahi kutokea katika kipindi cha zaidi ya miaka 50. Mafuriko haya yalitokea mwaka 1952; lakini mwaka huu wananchi wa Lindi wamekutana na mafuriko.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikwenda kuona eneo la tukio; lakini kuna watu ambao hawajaona hayo matukio. Lazima Mwenyezi Mungu tuwaombee wale wenzetu ambao wako katika mazingira magumu. Kitu ambacho hujakiona ni sawasawa na usingizi wa giza au usiku wa giza. Wenzetu wako katika mazingira magumu ambayo ukienda lazima utalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kilwa peke yake ni zaidi ya watu 15,000, Lindi takriban watu 8000 wako nje hawana mahali pa kulala, hawana kitanda, hawana godoro, hawana maji, hawana nguo, hawana chandarua. Sisi Wabunge Mungu ametupenda tumekaa humu ndani, tuko vyumbani tumelala, tumepumzika, tunashiba ndiyo maana kuna wengine wanabeza wakati mwenzangu kaka yangu Mheshimiwa Bungara anazungumza watu walibeza, msibeze, na ukibeza Mungu hataleta furaha katika nafsi yako.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna methali inasema kitu kimoja ukimkuta mtu masikini akikuomba pesa kama hauna pesa nyamaza, lakini kama unayo mpe kwa kuwa yeye naye anahangaika anataka kunusuru maisha ili apate rizki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetoka hapa kwenda Lindi na Nanjime nimekwenda Nanjilinji nimeshindwa kufika. Ina maana leo hivi kwenda Liwale huwezi watu wako katika kisiwa, kwenda Luwangwa watu wako katika kisiwa, kwenda Kilwa ndani vijijini watu wako katika visiwa, watu wanaokolewa na helkopta. Nimesikitika kuna mtoto anaitwa Derick Masanja huyo mtoto ana miezi 11; maana haya mafuriko hayakutokea wakati wa mvua yametokea wakati jua linawaka; maporomoko yametoka huko yamewakuta watu wakiwa mashambani, wakiwa na mifugo. Leo ninavyozungumza jamaa zangu Wasukuma ambao wametoka Ihefu hawana ng‟ombe, hawana mifugo yao, maisha yao ni magumu, hivyo tusibeze wakati wenzetu wakikuona kwanza wanaanza kulia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninalimba Bunge langu Tukufu kwa umoja tulio nao na huruma tuliyo nayo watakaokuwa tayari tuanze kuchangia tuwasaidie wenzetu. Huu ndio umoja ninauona mimi utatusaidia angalau kunusuru tuonekana na sisi Bunge tunaonekana tuna umoja na tunafarijika kwa kuwafariji wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo ninaingia katika hoja iliyokuwa mezani, nitazungumzia suala la maralia. Ukiachilia mbali UKIMWI malaria gonjwa ambalo linamaliza watu Tanzania, na bahati nzuri mwaka jana mwezi wa 12 nilihudhuria mkutano wa mabadiliko ya tabianchi (climate change meeting) ambao ilifanyika Madrid. Haya tunayoyaona walishayazungumza wenzetu mwezi wa 12. Walisema hivi; Afrika Mashariki kutatokea na maangamizi matatu; la kwanza mafuriko ambayo hayajawahi kutokea katika miaka mingi ndio haya tunayaona sasa hivi; lakini la pili kutokana na mafuriko haya na mvua za holelaholela mazalia ya mbu yatakuwa maradufu. Hivyo tutegemee ugonjwa wa Maralia ambao tulisema tunataka kuutokomeza bado tuna mkakati rasmi wa kuhakikisha maralia yamnatokomezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu tuko naye beneti katika suala la maralia, mimi ni Mwenyekiti wa Maralia; tuko nae kila siku yeye yuko kwenye kipaumbele kuhakikisha Tanzania yenye zero maralia inaanza na yeye na mimi nikifuatia na nyinyi vilevile mfuatie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kimoja nataka nimuambie ndugu yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Mheshimiwa Waziri, mikoa mitano mikubwa ambayo ina maralia ambayo ni high burden maralia ni Lindi, Mtwara, Geita, Kigoma na Kagera; lakini baadhi ya watendaji wanataka kuvuruga. Wametoa ajira ya kwenda kusaidia hiyo mikoa basi wameandika mikoa 10 ambayo imepewa kipaumbele, nataka nitaje kwa majina, Dodoma ambayo ina only one percent, Singida, Geita, Shinyanga, Kigoma, Katavi, Kagera na Mara; lakini Lindi na Mtwara hamna ilhali Lindi ina 24 percent. Sasa tujisikieje? Tujisikie sisi tuendelee kufa kwa ajili ya watendaji wachache wanaotuharibia program zetu za maendeleo ya kutokomeza maralia wanaiacha Lindi na Mtwara hamna? Kwa bahati nzuri mimi gazeti ninalo na nitakupa ulifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninaomba kitu kimoja, tu sitaki kubishana, naomba uiingize Lindi na Mtwara iwepo katika kundi la watu ambao ajira ipelekwe kwa watu kwenda kusaidia maralia hasa sasa hivi. Kutokana na mafuriko haya mimi nimekwenda site watoto wanatapika wanatisha. Ina maana wamekaa wanaumwa na mbu, hali ya maralia Lindi na Mtwara ni kubwa; na mafuriko yale kwa Lindi ina maana maralia kwao itakuwa ni maangamizo na vifo vitakuwa vingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaizungumzia suala la walemavu; Wizara hii ndio Wizara ya Walemavu. Tumepitisha sheria ya haki za walemavu lakini hakuna ajira ya walamavu. Walemavu wanaonekana ni kama kundi ambalo halistahili kupata ajira katika nchi hii. Tuna asilimia tatu ya walemavu tujiulize, Bunge lenyewe limeajiri walemavu kwa asilimia hiyo? Hapa ndani je, asilimia hizo zimetimia ina maana kwanza tujinyooshee sisi wenyewe ndani ya Bunge tunalitekelezaje suala la walemavu na ajira? Tunahitaji alama za sign language, hakuna Bunge. Watu wanakaa wanataka kuangalia Bunge linazungumzia nini, hakuna. Ina maana bado Bunge hawajajipanga kuhusu suala la walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Bunge kama Bunge tunaporidhia tuwe namba one kuhakikisha haki za walemavu zinaanza ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hapo tutasema kweli Bunge tumejisafisha ndipo tutake kusafisha maeneo mengine ya walemavu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele imegonga ya pili.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia tena kuhusu hao walemavu kwanza nishukuru Serikali….

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imegonga Mheshimiwa

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, haaa haijatimia!

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, shukrani.
Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru na niunge mkono kwa asilimia 100 azimio hili la kuunga suala la Selous. Nafikiri utaniatambua uwepo wangu katika miaka yote niliyokaa katika Bunge hili nikiitambua Selous ni pori kubwa sana na ni kubwa na linahitaji mapato ambayo yatasaidia kuchangia Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, umenipa dakika tano kwangu nitazifanyia kazi. Pori la Selous kwa ukubwa wake lina eka za mraba 154,000 ni kubwa zaidi ya Serengeti, Serengeti ni 12,500 ni zaidi ya mara 12. Sasa leo TANAPA mnavyompatia nafasi ndogo katika Pori la Selous atapata wapi mapato, maana yake atakuwa amehifadhi?

Mheshimiwa Spika, ombi langu la kwanza Selous yote iwe ndani ya Hifadhi ya Mwalimu Nyerere kwa sababu za msingi. Tuna corridor ya Nyasa Selous ambayo ya Tanzania, ile corridor lazima iwe potential kwa ajili ya ile wanyama wanapotoka Mozambique wakija Tanzania itakuwa tayari migration ile inafanyiwa kazi, nani ataifanyia kazi hiyo migration? Leo TANAPA ina mapori au hifadhi 16, lakini zinazofanya kazi ni nne tu ambayo ni Serengeti, Kilimanjaro, Mikumi na kidogo Manyara, mmeiongezea pori hili kubwa, mapato yatapatikana wapi?

Mheshimiwa Spika, naomba usimvalishe shati, mvalishe na suruali anataka awe suti na kama itakuwa ni suti tunahakikisha pori zima la Selous liwe na hadhi moja tu na ninaomba hadhi hii itengezwe katika mazingira matatu; yenyewe Selous kwa vile ni kubwa itengenezwe zone ya Kusini, ya Mashariki na ya Magharibi ambayo ni Matambwe.

Mheshimiwa Spika, mkilifanya Pori la Selous mmelimega sehemu ndogo mtaleta migogoro mikubwa sana ambayo mtashindwa kuiendeleza. Ombi langu tembo ambao wanamalizwa ndani ya Pori la Selous ili kuwalinda na kuweza kuzaliana na nchi kuweza kupata mapato ningeomba Pori la Selous liwe lote moja tu hakuna kubagua, kumega na namwomba ujumbe huu ufike kwa Mheshimiwa Rais, ananitambua kama mimi Mama Selous na kama ni Mama Selous ni lazima Selous iwe neno moja tu Hifadhi ya Nyerere basi, masuala mengine italeta missunderstanding kwa vile kutakuwa na mapato yanataka kuingia ndani ya Selous, hapa kumechukua hifadhi ndogo pale Kibiti au Rufiji, ni eneo dogo sana bado kuna migogoro mikubwa ya wafugaji ambao wako ndani ya Selous, sasa tutaifanya iwe hifadhi hakuna mfugaji mle ndani wala ukulima mle ndani wala uchimbaji mle ndani, utaifanya nchi ipate mapato makubwa.

Mheshimiwa Spika, wewe ulikuwa Liwale unaijua Selous kwa undani wake. Leo Selous hii kuimegamega ni tayari unaitengenezea mazingira magumu na TANAPA mtawapa mzigo ambao watashindwa kuutengeneza. Leo TANAPA inaweza kuingiza mapato makubwa, lakini mapato yale kama hamjayatengenezea mazingira yake mazuri ina maana mtaifanya TANAPA iwe paralysed.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme tena kusema Pori la Selous kuliweka katika hifadhi mmeiingizia uchumi nchi, ile migogoro tiliyokuwa tukizungumza kila siku na kelele tulizokuwa tunapiga sasa hivi tutakuwa tumemaliza kabisa. Matumaini yangu nendeni mkakae, mkajitathmini je, kwa nini tuchukue sehemu ndogo wakati Selous yote ile ni kubwa pori zima liingie katika hifadhi, msibague…

MHE. CHACHA R. MARWA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa, endelea.

T A A R I F A

MHE. CHACHA R. MARWA: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji mama yangu, ukichukua Selous yote uifanye kuwa National Park utakuwa hujaisaidia, chukulia tu mathalani Serengeti National Park imezungukwa na game reserve, imezungukwa na WMA, hizi hapa ni zile ambazo zinasaidia pia wananchi ambao wanazunguka, ili kuona ya kwamba hii national..., kumbuka National Park huwezi kuwinda, huwezi kufanya chochote zaidi ya kupiga picha, lakini unapokuwa na game reserve pembeni unaruhusiwa kuwinda na kuvuna wanyama.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa nataka tu aone kwamba hili jambo lina umuhimu kwamba, sehemu iwe National Park na sehemu nyingine iwe game reserve kwa ajili ya kusaidia wananchi wanaozunguka. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Unaipokea hiyo taarifa, Mheshimiwa Riziki?

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, siipokei kwa vile hajitambui na hajui ninachokizungumzia ni nini, mimi nazungumzia mapato ya nchi, yeye anazungumzia ubinafsi na inabidi akalisome Pori la Selous ajue maana yake ni nini na potentiality ikoje. Na toka tumeanza uwindaji hakuna faida tunayoipata, tunataka Selous iwe ya mapato na maendeleo sio mabishano hapa tunataka kuijenga nchi, tunataka kumsaidia Rais, tunataka kumfanya Rais wetu aweze kutukuka ajue anachokifanya ni nini. Sio kutaka kuleta ushabiki wa kisiasa.

Mheshimiwa Spika, hapa mimi sizungumzi siasa, ninazungumzia uchumi wa nchi ambao utaifanya nchi yetu iweze kupaa na Rais vilevile anachokifanya wao ambao walikuwa wanapingana nae anataka kuiweka nchi ikae katika reform, hivyo sikubalianinae na ninaomba aje nimuekeleze ajue mimi Mama Selous naijua Selous kwa undani wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza hayo niiunge mkono hoja na ninasema tena ninawaunga mkono kwa vile leo TANAPA inapewa mzigo mkubwa sana. Sasa tutapompa Selous ambayo haina potential kama ilivyo kwa Kitulo, Kitulo imepewa katika hifadhi haina potential, Katavi iko katika hifadhi haina potential, Buruwando iko katoka hifadhi haina potential, Gombe iko katika hifadhi haina potential, haya tunakwenda maeneo mbalimbali ya hifadhi ambayo wamepewa hayana potential wanategemea maeneo manne tu na Selous kwa vile yana potential na Selous watalii wanaijua kama Selous ni eneo potential.

Mheshimiwa Spika, ni Serikali ya kusimama kuwahakikishia dude hili tunalifanyaje ili iingize mapato. Masuala ya ushabiki, siasa, hakuna, hapa tunataka uchumi ambao utakuwa endelevu na utamsaidia Rais Magufuli katika maendeleo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hapo nawashukuruni sana. Ahsanteni sana. (Makofi)
Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na mimi kuipata hii nafasi, lakini ninaiunga mkono kwa asilimia mia moja kwa vile huu mkataba au hili azimio itaisaidia kuifanya nchi iondokane na athari ambayo ilikuwa tayari inaangamia kutokana na climatic change au mabadiliko ya tabianchi ambayo Tanzania ilikuwa mojawapo ya nchi ambayo inaingia katika maangamizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufanya hizi Hifadhi ya Ugalla na Hifadhi ya Kigosi kuingia katika hifadhi sababu zake kwanza Tanzania ilikuwa tayari misitu inatoweka, Tanzania wanyamapori walikuwa wanatoweka, hata uoto wa asili ulikuwa unatoweka, sasa kitendo cha kujikuta leo tunaazimia hili azimio ni imani yangu kuwa sasa hivi tunakwenda kubadilisha mazingira ambayo yalikuwa nchi inakwenda katika jangwa kuirudisha katika nchi ya kijani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe ni shahidi, Mikoa ya Singida, Dodoma, Shinyanga, Tabora kote huko ilikuwa tayari kumeshaingia jangwa kubwa sana kwa ajili ya watu walikuwa wanakata miti na ilikuwa sasa hivi mpaka Mikoa ya Lindi, Kusini kote misitu inatoweka, lakini sasa hivi TANAPA ina mbuga 20 wana matatizo makubwa ya kutozwa kodi nyingi ambazo zimeingizwa mle ndani. Je, mmewapangiaje kuwaondolea hizo kero ambazo itaifanya kuzitengeneza hifadhi zingine ambazo hazizalishi ili kuifanya hizi hifadhi zingine ziweze kuzitegemea zile hifadhi ambazo zinazalisha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, leo hatuitegemei Ugalla katika muda mfupi huu kuweza kuzalisha wala Kigosi, Burigi na hizi hifadhi mpya hii ya Selous, lakini mkiwatengenezea mazingira ambayo itaifanya hii taasisi iweze kujiendesha mtakua mmefanya vizuri sana, lakini si hivyo tu, kuwaweka viongozi ambao wana uwezo. Tumezoea kuwaweka watu ambao hawana uwezo matokeo yake baada ya muda watu hawa watatoweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo, Director General wa TANAPA amepewa hifadhi 20 kwa kweli tumpigie makofi huyu baba amefanya kazi ya ziada sana, ameweza kuifanya TANAPA kuweza kupata mapato na nchi hii kujivunia TANAPA kama eneo la kujivunia. Je, mmempa hizi hifadhi, mmemwekeaje mazingira yake, anastaafu niliongea katika Bunge lililopita, kama anastaafu mmejipanga vipi hao wanaotaka kuja ili angalau awaachie watu ambao mfumo mzuri ambao aliuendeleza ili uweze kuendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mategemeo yangu kuwa Serikali isiangalie watu kwa ajili ya uzee, angalia leo Malaysia watu wazee ndio wanaiongoza Malaysia, siyo lazima kila mahali iwe kijana, hata mzee ukimuongezea muda akaisimamia hiyo kitu mtafikia mahali nchi hii tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumzia suala la zebaki, hili azimio ni zuri, kwa sababu wachimbaji wadogo wadogo wote wanafanya uchenjuaji wao kandokando ya mito na kandokando ya mito tunategemea binadamu wanakwenda kulima, tunategemea kwenda kuchota maji kandokando ya mito, tunategemea wanyama kandokando ya mito kwenda kunywa maji, sasa contamination hii ya madawa ambayo yanatumika ya zebaki inatufanya Watanzania wengi tunaathirika, tuchukue Mikao ambayo kuna wachimbaji wanahamahama kila siku, athari yake si ndogo, ina maana miti yetu, mito yote inaingia katika maji machafu lakini siyo sababu lazima tupange mpangilio ambao na hawa wachimbaji wadogo wadogo, kwa vile ndiyo maisha yao, tuwe tumewawekea mazingira gani, lazima tuwe na shughuli mbadala ya kuwakabidhi au kuna kitu mbadala cha kuwasaidia hawa watu ili na wao wasiendelee kuwa maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana katika masuala ya mazingira, Serikali tuisimamie, tulikuwa na asilimia 20….

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru na mimi kupata nafasi ya kuchangia katika hoja iliyokuwepo mezani; nitachangia michezo pamoja na walemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania imeridhia haki za walemavu ndani ya Umoja wa Mataifa, na katika eneo ambalo inabidi lifanyiwe kazi ni utalii ndani ya Umoja wa Mataifa. Katika takwimu tulizonazo za dunia walemavu tuko asilimia 15, na katika kuwa asilimia 15 walemavu wale wanahaki ya kufanya utalii katika nchi yetu ya Tanzania. Ndiyo maana leo mmewaona Tembo Warriors wamekuja hapa kuja kuwawakilisha walemavu na kumtangaza Tembo katika nchi yetu ya Tanzania. Kila Mtanzania anatakiwa kusema say no to poaching; ujangili basi, imetosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanini nazungumza hivi kila mwaka Kenya wakiwa katika mkutano wa UN wanasema come and visit Kenya and visit Serengeti, and visit Ngorongoro and Zanzibar. Kwanini, wenzetu wako wanajitangaza. Mimi leo nasema nimejitolea ninataka kusimama kwa hili nikishirikiana na mashirika yote ya utalii ya TANAPA na Ngorongoro watushirikishe na kumpa bendera Mheshimiwa Ikupa aende UN akatangaze utalii ndani ya UN. Naomba Wizara tatu za kushirikiana nazo zimpe ushirikiano Ikupa. Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje, Wizara ya Maliasili na Utalii na Ofisi ya Waziri Mkuu impe ushirikiano Ikupa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina sababu za msingi; kule ndani ya Mkutano wa UN kuna event inafanyika katika kila nchi, state parties. Si kila siku Ikupa atakwenda Marekani anakwenda kufanya nini; tunataka akapeleke ujumbe kama Tanzania yenye utalii na walemavu inawezekana. Na walemavu waliokuwa kule ni maprofessor, wafanyabiashara; ina maana hii 17 percent ambayo ni point two mnaitegemea, tunauwezo wa kuiongezea na iwe hela nyingi zaidi katika suala la utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninaona katika Bunge hili walemavu tunazidi kuongezeka Mheshimiwa Kigwangwala sasa hivi ni mlemavu wa matatizo ya mikono, tunakukaribisha katika kundi la walemavu, karibu sana unakaribishwa, Mheshimiwa Kanyasu ukiwa mrefu sana na ukiwa mfupi sana vile vile nalo lina matatizo kidogo ya kiulemavu ulemavu ulemavu; na wewe vile vile katika kundi letu la walemavu na mtuunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lile desk linafurahisha, ina maana tutawaunganisha walemavu ambao watahudhuria katika mkutano ule na kuwaambia Tanzania kuna utalii. Juzi ilikuja meli na watalii 2500 wameshindwa kushuka Dar es Salaam kwa vile hakuna mazingira ya walemavu wale kuingia Dar es Salaam. Kurudia makosa ni kosa lakini sisi tunataka kusema kwamba kuanzia leo Jiji la Dar es Salaam lianzishe mradi wa city tour ili walemavu waweze kupata uwezo wa kutembelea Jiji la Dar es Salaam. Nina imani Mkurugenzi wa Dar es Salaam Mama Spolar Liana amelianzisha hili, mpeni ushirikiano Spolar aanzishe utalii Dar es Salaam ili watalii wa kawaida na walemavu waanze kuingia Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe pongezi zangu za dhati. Kwanza nimpongeze Allan Kijazi, nimpongeze Manongi kwa kweli mimi sina cha kusema; hawa watu wameweza kusimamia mifumo mizuri ndani ya Mashirika haya. TANAPA sasa hivi inaweza kutoa milioni 37 ndani ya Serikali kama ruzuku, na bilioni 20 kusaidia miradi mbalimbali kwa Tanzania hii. Pia Ngorongoro ni hivyo hivyo, wameweza kupeleka Serikalini; wamevuka malengo wamepeleka bilioni 22. Mashirika mengi yanachukua ruzuku ya Serikali lakini hawa wameweza kutengeneza mifumo mizuri ambayo Serikali badala ya kuwalipa wao, wao wanaipelekea pesa za ruzuku ili kuuendesha utalii na uweze kuwa endelevu na nchi kupata uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingekuwa nchi nyingine hawa watu wangepewa nobel, na mimi bila kusema chochote nasema ninawapongeza. Kwa niaba ya walemavu wenzangu na baadhi ya walemavu wenzangu na baadhi ya wapenda maendeleo ya utalii nasema Ngorongoro kwa kupitia Manongi na Mr. Kijazi, Mungu awabariki. Wanakaribia kustaafu, na kama wanastaafu wawaandae vijana ambao watashika ule mfumo usiharibike. Ule mfumo ulioko kule umeifanya sasa hivi Serikali inapata mapato yake bila kuwa na matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilizokuwepo; kuna changamoto ambayo ng’ombe ukimkamua sana huyu ng’ombe ataharibikiwa. Wakiondoka Kijazi na Manongi tunaweza tukaiona TANAPA na Ngorongoro zinakufa. Serikali naomba isimame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Wizara ya Fedha kuna tozo zinatozwa ambazo zinazifanya taasisi hizi zisijiendeshe. Wanahitaji barabara wanahitaji mifumo ya maji, wanahitaji mifumo ya mawasiliano wanahitaji kupata mishahara kwa wafanyakazi. Sasa Serikali inayotusikiliza, wanasema Serikali sikivu na mimi nasema ndiyo; naomba wawaangalie na hizi tozo zilizopo mziangalie kwa makini msije kuiue TANAPA na Ngorongoro ili baadaye mashirika haya yapewe ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuja kwenye hoja ya pili. Kuna uchonganishi; unazungumzia mikoa ya kusini ni Lindi, Mtwara Ruvuma, ukizungumzia Nyanda za Juu Kusini ni Iringa, Mbeya Katavi na Sumbawanga; na hii imekuwa ni mazoea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umekuja mradi wa SAGCOT (Southern Agricultural Corridor of Tanzania) Lindi, Mtwara Ruvuma hatumo. Mradi huu umepita, watu wamenufaika, mikoa imenufaika sisi hatukunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umekuja mradi wa World Bank kuna haja gani kusema mikoa ya Kusini? Definition ya Mikoa ya Kusini iko wapi ilhali Lindi na Mtwara hatumo? Ina maana mmetuweka sisi kikaangoni tukingojea mikoa mingine ikipata maendeleo sisi tukiendelea kuswaga kuwa masikini na ilhali tunaongoza kwa utalii mkubwa kuliko mikoa mingine yoyote? Nataka niiorodheshe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pesa ya Kilwa ya mwaka 1000 leo imeonekana Australia nchi ilipokuwa inajitegemea. Katika urithi wa dunia Kilwa iko namba 21, lakini katika urithi wa dunia huu utashangaa katika mradi wa kusini Lindi, Kilwa, Mtwara Ruvuma mpaka Namtumbo hazimo. Sasa tunafika mahali tunajiuliza hawa wataalam nafikiri wanatufanya sisi tuwe na chuki na mazingira haya. Haiwezekani leo utalii mkubwa wa Selou, maana Selou kutokea Kingupila kwenda Lindi tunachukua two third; Matambwe iko Morogoro na Morogoro iko Mashariki hivyo usichanganye na Kusini. Hivyo kama unaipeleka Matango, Udzungwa na Mikumi haiko Kusini kabisa. Leo tutajivunia nini Kusini na utalii wa Kusini? Hatumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivutio vikubwa vilivyokuwa kusini, kwanza corridor ya Selous Niassa, Mozambique, ile corridor ni ya tembo, mbwa mwitu, samba nyati. Nimepiga kelele mpaka leo sioni kama kuna majibu ya kueleweka. Lakini nilikwenda mimi; niishukuru taasisi ya GIZ ilinipa nafasi ya kutembelea na baadhi ya waandishi wa habari; zile corridor wanazopita tembo tayari wafugaji ambao wametolewa Ihefu wamevamia; na baada ya kuvamia mnataka kuhalalisha ili viwe vijiji vya asili; maeneo wanapita tembo unahalalisha kuna nini hapo? Tunaji-contradict.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ninaomba ujumbe huu ninaotoa sasa hivi umfikie Mheshimiwa wangu Rais kwa vile jamaa zake ndio wanafujo ya kupeleka mifugo katika maeneo hayo na wanaingia na magobole. Hivyo tutakapowamaliza hawa tembo na simba utalii utakwisha. Simba anatoka Mozambique anaingia Selou anaingia Tunduru, anaingia Masasi, anaingia Masasi Liwale, anaingia Matambwe, anaingia Mikumi anaingia Kilosa, anaingia Mkungunero, anateremka Ngorongoro, anakwenda Serengeti anakwenda Maasai Mara. Njia hizi mkiziharibu hawa wanyama watapita wapi? Binadamu wamevamia haya maeneo na katika kuvamia maeneo haya ilikuwa only 20 percent ya hifadhi katika Tanzania inakwenda kwa wanyama. Sasa hivi tumepunguza na tuko chini ya 15 percent. Tukizidi kupunguza tunaisaidia nchi au tunaiharibu nchi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango wako mzuri.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nikushukuru na niwatakie heri Waislam na wasiokuwa Waislam katika mwezi huu Mtukufu na kuwaombea amani na utulivu katika nchi yetu ya Tanzania ambayo itajengwa na Watanzania wenyewe. Hawezi kutoka mtu huko nje kuja kutuletea amani na utulivu, tushikamane Watanzania wote, tuijenge amani yetu na wenzetu wajifunze na iwe mfano katika nchi za wenzetu ambao wameonja vita ikiwemo Libya. Libya wameonja vita wakasema hakuna democracy, leo wenzetu wa Libya wapo katika uchumi mgumu, tujifunze kwa mapana yetu, tusiende kuhangaika na maneno ya uchochezi wakaifanya nchi ikamwaga damu. Nawapenda Watanzania, naipenda amani ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nitazungumzia suala la mjusi ambaye yupo Ujerumani. Nilimwacha katika Wizara ya Maliasili kuileta kwa vile hapa ni sehemu pekee ambayo Ubalozi wa Ujerumani ni kama nchi ya Ujerumani iweze kutuambia sisi watu wa Mkoa wa Lindi ambao lile jusi kubwa (dinosaur) na mifupa yake ipo Ujerumani, tunapata nini ndani ya yule mjusi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimetaka kufunga ukurasa leo, Wizara ya Maliasili, Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ishirikiane na nchi ya Ujerumani tuweze kujua katika Halmashauri ya Lindi inapata nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji ambavyo vimezunguka pale palitoka yule mjusi wamesema it’s a lost science, hapana it’s a life science. Naomba Ubalozi wa Ujerumani wawatoe wawakilishi, nifuatane nao mimi nikiwa na kundi langu maalum twende mpaka Tendeguru lilipotoka lile jusi ili wakajionee kuwa jusi lile limetoka Tanzania katika Wilaya ya Lindi Vijijini, katika Kijiji cha Mipingo na Wanamipingo waweze kufaidika na mjusi yule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili nalizungumza kwa mapana yake; utalii mkubwa utakaopatikana ndani ya Tendeguru utakuwa ni uchumi mkubwa katika uchumi wetu wa Tanzania. Tulikaa kwa muda mrefu toka mwaka 1905, mvumbuzi ambaye alikuwa mchimbaji wa madini akishirikiana na Wolf Henrick pamoja na Martin Abald, wao walikwenda Tendeguru kuchukua ile mifupa kwa ajili ya uchimbaji, wamepeleka Ujerumani, kunafanyika exhibition. Katika miaka yote mpaka leo katika vijiji vile hatujafaidika hata kwa kujengewa shule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini yangu Balozi na wawakilishi kutoka Ujerumani wananisikia, tukitoka hapa moja tu kuwa tunataka maendeleo katika Wilaya ya Lindi katika kupitia eneo lile lililotoka mjusi hata angalau wakatuonyeshe kumbukumbu iko wapi. Tunataka ushirikiano kati ya Ujerumani na Lindi Vijijini ili angalau Lindi Vijijini wajue pato linalopatikana na wao wanafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu; naomba tupate shule katika eneo la Mipingo na vijiji vinavyozunguka, tunataka maji maana yake maeneo yale hayana maji, tupate maji katika maeneo yale, tupate vituo vya afya ili kujenga uhusiano bora uliokuwepo kati ya Tanzania na Ujerumani kwa kupitia dinosaur. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho, wanazungumza halijulikani it’s a lost science, it’s not a lost science, it’s a life science come to Tanzania and visit Tendeguru na mtaona kila kitu kipo pale. Ni matumaini yangu kuwa leo naitangaza Tendeguru ndani ya Bunge, naitangaza Tendeguru ndani ya Ujerumani, Wajerumani tukutane baada ya Bunge, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje, Waziri wa Maliasili na Waziri wa Fedha tukutane kwa pamoja na mimi mwenyewe kama mdau mwanaharakati kwa muda wa miaka 15, naomba nami niwepo nithibitishe hili ili mapato yapatikane na nchi yangu iweze kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia fursa zilizopo ndani ya Balozi zetu. Nchi hii tuna Balozi ambayo inataka kutupa uwakilishi, wale Mabalozi wasikae ubalozini kule wamekaa wanatumia pesa nyingi, matumizi makubwa. Je, wana-deliver nini katika nchi yangu ya Tanzania? Tunataka fursa tulizokuwa nazo Tanzania za kilimo, madini waje watuonyeshe tunafanya hivi. Tumekwama tunataka soko la Euro, wale wa Europe wanatupa soko gani sisi Watanzania ili angalau tutoke na mazao yetu, haiwezekani Tanzania soko letu mpaka twende Uganda, Rwanda; imekuwaje Mabalozi wetu wanafanya nini kutushirikisha kama nchi kuiingiza katika uchumi bora wenye maendeleo. Tanzania yenye maendeleo kwa kupitia Balozi zetu inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru sana na nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyenijaalia afya njema nikaweza kuchangia katika hoja iliyokuwepo mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli kwa huruma na upendo mkubwa aliouonyesha na kuweza kunichagua kuwa Mbunge wa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais. Nasema Mwenyezi Mungu ambariki na sina la kusema zaidi ya kuendelea kumuombea Mwenyezi Mungu aweze kumtetea na aweze kumlinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru wananchi wa Mkoa wa Lindi kwa maombi yao na Watanzania kwa ujumla, nasema ahsante. Mwisho, nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa upendo walionionyesha na hata mimi kunipa moyo na kuniongoza na kunifikisha hapanilipofikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti,nina hoja ambayo ni ya muda mrefu, lakini Mheshimiwa Rais baada ya kunichagua nimeona nije na hoja yangu. Naomba Wabunge wenzangu mniunge mkono na muitambue kama hoja hii ni kwa maslahi mapana ya nchi yangu.Mwaka 1905 mpaka 1906 katika eneo la Tendeguru, Wilaya ya Lindi Vijijini, Mkoani Lindi walichukua mabaki ya mjusi kupeleka Ujerumani. Mwanzo nilikuwa nadhani ni mabaki yale ni ya mjusi mmoja, kumbe na mijusi sita, lakini nazungumza kwa uzalendo na uchungu wa kuhakikisha haya mapato ni lazima yawasaidie Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama mimi sitatumia lakini kuna watu wanahitaji mapato hayo kwaajili ya elimu, barabara, afya na kadhalika. Ujerumani wamepeleka lile jusi na Watanzania kutoka Lindi walilibeba kichwani jusi moja lilikuwa na uzito wa tani 250 kutoka Dendeguru mpaka kufika Kilwa tu kwenye Bandari, basi ujue wametembea kilomita 150, wametesekaje watu kama hawa, wengine wamepoteza maisha yao ukichukulia kipindi hicho kilikuwa ni kipindi cha wanyama wakali; je, wale wananchi wa kule wameangaliwaje, hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti,Tunaambiwa kuwa wao kwa mwaka wanakusanya Euro milioni 278, ukifanya calculation za haraka ni sawasawa na bilioni 834, sisi kama Tanzania hatujapata chochote. Ukiwauliza wanasema zile pesa zimejenga museum kule kwao, zinatumika kuwalipa mishahara watu wanaomtunza, zinalipa hela za tafiti mbalimbali, zinawawezesha wanafunzi wanaokwenda pale kujifunza wanatumia nafasi ile. Nasema haiwezekani na wanasema wameingia mkataba na Umoja wa Mataifa kuwa haiwezekani huyo mjusi kumrudishaTanzania, hakuna kisichowezekana katika ulimwengu huu wa Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabilioni yale 834 wanayoyavuna Wajerumani hata kule anapotoka mjusi yule hawapathamani. Sisi Tanzania ndio owner wa yule mjusi na Watanzania mfunguke na siyo kila wakati mnataka kubeza, mbona kama mngekuwa naye Tanzania msingeweza kumfanyia chochote, je, kama nao wangemwacha wangefaidika, wasingefaidika naye. Ina maana kuwepo kwa mjusi yule kwao ndiyo wamefaidika. Leo dunia unaisikia inavyozungumza wanaitegemea Afrika ife ili wachukue rasilimali zetu na walikwenda pale kuchimba madini. Hivyo Ulaya unayoiona, dunia ya kwanza unayoiona ilitajirika kwa kupitia Afrika. Wametegemea dhahabu, almasi, copper, zinc, shaba kutoka Afrika lakini sisi wenye Afrika hatujitambui na wala hatujielewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao, wanahitaji viwanda vyao vifanikiwe na ili vifanikiwe wanahitaji raw material kutoka Afrika. Ndiyo maana Mheshimiwa Rais anasema tunahitaji viwanda kwa ajili ya kuleta mabadiliko ya nchi yetu. Haya mazao yetu badala ya kupelekwa Ulaya yatafanya kazi hapa hapa tutawapelekea vitu ambavyo tumevi-process Tanzania. Tuangalie kipindi hiki tunachokizungumza cha Corona hatuwezi kuleta chochote kutoka nje lakini kama viwanda vyetu vingefanya kazi, nani angeagiza khanga kutoka India au China, tungekuwa na khanga zetu kutoka urafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya mjusi tumeunda Kamati, naomba uridhie na uingize ndani ya Hansard na uitambue kama Wabunge wako wamejitolea rasmi kuhakikisha haya mapato yanakuja Tanzania. Nataka niwatambue Wabunge ambao wako tayari akiwemo Mheshimiwa Kigua, Mheshimiwa Reuben Gwagilo, Mheshimiwa Ritta Kabati, Mheshimiwa Juma Hamad, Mheshimiwa Maimuna Patani na wengine watakaojitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji mapato yaje Tanzania na siyo mapato tumekwenda kufanyiwa presentation Wizarani neno la kukatisha tamaa la kwanza wanasema haiwezekani hata mfanyaje mkafanikiwa. Mimi nasema inawezekana na tutafanikiwa. Lugha ya kukatishana tamaa Tanzania tuiache. Katika maisha yangu sina uwoga, nikipambana na kitu changu nasema hiki kitu kitafanikiwa na nasema nitafanikiwa. Ndiyo maana nakwenda sambamba na nyayo nafuatilia miguu step by step ya Mheshimiwa Rais kwa ajili ya mafanikio. Mheshimiwa Rais hana woga, ametishiwa sana, ameambiwa sana kuwa haiwezekani lakini yamewezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hoja ya madini imewezekana na hii hoja nahakikisha kuwa itawezekana. Nachoomba ni ushirikiano wa Wizara mbalimbali zinaguswa na hoja hii. Kama waliona mapambano haya hayawezekani hata kama mimi naondoka lakini bado kuna wanaharakati wako humu ndani ya Bunge ambao watakwenda sambamba na tutashinda vita hii na kuiletea mapato nchi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alinipigia simu Balozi akaniambia Mama Lulinda usirudi nyuma na mimi nimemwambia niko na wewe sirudi nyuma. Ananiambia panafanyika mafunzo mbalimbali ya watu duniani kwenda kusoma kwa nini mjusi ile mikubwa imetoka Tanzania, sisi wenyewe Tanzania tuko wapi? Hatupo! Tuna watoto wamesoma wanahitaji kwenda kufanya exchange program kwa nini wanawachukua watoto kutoka Marekani, watoto wa Tendeguru wako wapi? Kuna watoto wamemaliza shule tunataka Wajerumani wakawasomeshe watoto wale ili tukijenga Museum kule Tendeguru basi na wao wawaeleze hapa ndipo palitoka fossil za mjusi kutoka Tanzania. Hivyo exchange program ya elimu naomba iwepo katika mkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili, watu wa University of Dar es Salaam wanakwenda kuchukua fund kwa ajili ya kufanya research…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia ni dakika moja Mheshimiwa Lulida muda umeisha malizia.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Niendelee?

MWENYEKITI: Malizia maneno yako ya mwisho.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa research University of Dar es Salaam wanachukua pesa, watu wa Makumbusho wanachukua pesa lakini wanachukua fund zile bila kuwa na utaratibu. Nachoomba sasa hivi pawepo na utaratibu Wajerumani waje kukaa na Tanzania tuwe utaratibu maalum haya mapato yaweze kuisaidia nchi yetu. Kwa mwaka wanapata Euro milioni 278 sawasawa na bilioni 834 Tanzania tunapata nini? Tunaomba Wizara…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Riziki Lulida.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana na nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyenijaalia kunipatia afya njema na kuwaombea Wabunge wenzangu Mwenyezi Mungu awabariki sana tusimame kwa pamoja tuweze kuwasaidia wakulima ambao wengi wanahangaika na wakiwa katika mazingira magumu ya mafanikio yao. Msimamo wa Wabunge kuwasaidia wakulima utainua uchumi na kumsaidia Rais wetu katika kuleta maendeleo yaliyokuwa ya kweli.

Mheshimiwa Spika, bado ni mtoto ambaye nimezaliwa katika zao la korosho, korosho ndio zao la kwanza toka tumepata uhuru ukichukulia madini tunaweza kupata fedha za kigeni. Kutoka mwaka 1961 tunapata uhuru mpaka mwaka 2017 zao la korosho lilichezewa danadana sana, tulikuwa tunapata haizidi bilioni 141. Lakini mwaka 2017 baada ya kusimamia mifumo na kuona hapa tunapigwa tuliweza kuuza korosho kwa dola milioni 530 tukapata trilioni 1.2 ikaitwa dhahabu ya kijani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii dhahabu ya kijani haikuja hivihivi, ilikuja kwa kusimamiwa; tujiulize kwa nini tuliweza kuleta mafanikio ambayo yalichezewa kwa muda wote pana kundi hapa linacheza na wakulima ambao hawawatakii mema wakulima.

Mheshimiwa Spika, wakulima hawa unaowaona wanapalilia mashamba yao kwa hela yao, wananunua pembejeo kwa hela yao lakini siku ya stakabadhi ghalani mabenki yote yapo pale na wafanyabiashara wote wapo pale wanataka kuhakikisha mkulima huyu kazi aliyoifanya wao wawe wanufaika zaidi kuliko wao, haikubaliki. Huu ni unyonge wametufanyia kwa miaka mingi hatukubali, nataka niwe mkweli na ni mzalendo wa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna lugha wanazungumza wafanyabiashara wanaonewa, sikubali kama wafanyabiashara wanaonewa, wanaoonewa katika kilimo ni wakulima sio mfanyabiashara. Kama tuliwezanyonywa kuhakikisha tunapata bilioni 141 zaidi vis-a-vis ya trilioni 1.2, nani alimuibia mwenzake hapa? Aliyeibiwa hapa ni mkulima. Watanzania tufunguke, hali ya uchumi wetu tunaweza kuusimamia na tukaweza kutoka hapa, tuache longolongo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viwanda, biashara na kilimo vinakwenda sambamba; leo enzi ya Mwalimu alitengeneza mifumo ambayo tungeenda nayo mpaka sasa hivi tungeruka. Mikoa yote inayolima korosho tulikuwa na viwanda, viwanda vyote vimefungwa mpaka leo hatujui mwisho wake ni nini. Tumemnyima ajira Mmakonde, Mngoni, Myao na mtu wa Liwale kwa ajili ya uhuni wa kibiashara halafu mnasema wanaonewa,nani anamuonea? Tuachane na lugha ambazo zinatufanya tuna- paralyze katika akili na mifumo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeonewa sana katika kilimo halafu bado wameonewa, wameonewa; amemuonea nani, wao walizoea kutuonea. Korosho ilikuwa inauzwa shilingi 600 lakini ghafla mwaka 2017 korosho iliuzwa 3200, nani alikuwa anamuonea mwenzake? Na hiyo 600 kuipata kamilifu haiwezekani, tukapata hela ya mfuko. Mfuko wa kwanza ilikuwa bilioni 97 macho yalianzia hapo, baada ya kuona bilioni 97 pakaleta siasa za uongo na vitu mbalimbali ambavyo vilifanya zile hela hazikumsaidia tena mkulima, korosho imeanguka chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mikoa iligawanyika kwa ajili ya mazao yanayolima, kahawa Kilimanjaro, Kagera na Mbeya, korosho Lindi, Mtwara, Ruvuma na Pwani tuendeleze hapa kwanza na mikoa ya Tanga ya Pwani ambayo hali ya hewa yao inakwenda sambamba na korosho. Leo tumeitoa korosho tukapeleka sehemu ya baridi unafikiri korosho inastawi, haistawi, itaota lakini haitakuwa na yield ya kutosha. Sasa hela zikagawanyishwa peleka huku, peleka huku matokeo yake mkulima wa korosho aliyesafisha shamba na kutafuta pembejeo yeye mwenyewe inapatikana hela hana thamani tena, hela ya mfuko inapelekwa sehemu zingine mkulima wa korosho ameachwa anahangaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nililizungumza viwanda vilifungwa makusudi na wawekezaji na wawekezaji wapo humu ndani ni wafanyabiashara, wamevifunga mpaka leo havifanyi kazi maana yake hakuna ajira kusini. Tuambieni kusini kuna kiwanda gani, Mkoa wa Lindi, Mtwara na Ruvuma hakuna viwanda nenda Tunduru viwanda vimefungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili achukue ile korosho anaipeleka nje kama as a raw material, malighafi na kule anapopeleka anasimamia kwa viwanda vya kule vitafanya kazi na itatoa ajira kwa watu wa kule sio kwa ajili ya mtu wa kusini. Tujiulize tunafanya nini, Watanzania tunasomesha vijana wana degree mbalimbali za kilimo lakini unaona bado tunahangaika na kilimo.

Mheshimiwa Spika, tunaomba viwanda vya korosho vifunguliwe tupate ajira ili matatizo ya kutaka korosho ile kuipeleka nje wanaotufanyia baadhi ya wafanyabiashara korosho ya Tanzania italiwa na Mtanzania humuhumu ndani na brand itatoka Tanzania. Leo brand ya korosho inatoka Sri Lanka wewe hujawahi kusikia vitu kama hivi; kahawa ya Tanzania inakuwa branded Uganda, parachichi la Njombe linakuwa branded Kenya, tuko wapi? Unaletewa wataalam wa shamba shape kuja kutusaidia kutoka Kenya, hivi hatuna vijana tuliowasomesha wanaojua suala la kilimo, tume- paralyze. Na kama hatujifungui kwa hilo nakwambia tutaendelea kupiga kelele na siasa ambazo hazitamsaidia mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkulima anahitaji akombolewe, tulijua kuanzia mwaka 2017 tumeshatatua tatizo la korosho tungekwenda kwenye kahawa lakini leo kahawa ya watu wa Bukoba inauzwa Rwanda na Rwanda wanapata uchumi kwa kupitia mazao ya Tanzania, sisi wenyewe tupo wapi? Tunasema tuna asilimia 29, haiwezekani, hii ni asilimia ndogo sana sio ya kuridhika na kufurahia nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ufuta; zao la ufuta la pili…

SPIKA: Mheshimiwa Riziki muda haupo upande wako.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipatia hii nafasi. Vile vile nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia sisi hapa angalau kupata uhai na afya njema, tunasema ahsante Mungu. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi anayoifanya kama mama mwenye upendo kwa kuhakikisha maendeleo ya Tanzania yanapatikana na juhudi kubwa anazozifanya na sasa hivi hata sisi akinamama tunapata nguvu kuwa tunaye Jemedari wetu ambaye anapambana na uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitazungumzia upandw wa Bandari, katika njia kuu nne za uchumi mojawapo ni bandari. Toka enzi ya ukoloni walifanya utafiti mkubwa sana wa kuona mafanikio ya bandari zetu hasa Bandari ya Mtwara, Bandari ya Tanga na Bandari ya Dar es Salaam; nitajikita katika Bandari ya Tanga na Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona leo hizi bandari zikiwa zimeachwa hazina kazi ya kufanya wakati tunahangaika na mizigo katika bandari hii ili kuleta pato na kodi kubwa katika uchumi wa nchi yetu tutaanzia na bandari wa Mtwara, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutoa tamko kuwa Korosho zote zinazotoka Mikoa ya Mtwara na Lindi zinakwenda katika Bandari ya Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mafanikio makubwa sana kuifanya ile Bandari itakuwa inafanya kazi lakini vile vile sio zao la korosho tu tunataka hata kahawa ya Mbeya, kahawa ya Ruvuma yote iende katika Bandari ya Mtwara. Nilikuwa naangalia kilometers za kutoka Ruvuma mpaka Bandari ya Mtwara. Kutoka Ruvuma-Songea mpaka Mtwara ni saa 8.53 na kutoka Ruvuma au Songea mpaka Dar es Salaam ni saa 14.53 ina maana ni masaa 15 ukiachilia mbali foleni za Dar es Salaam lakini utashangaa kahawa ya Mbinga badala ya kuipeleka Mtwara inapelekwa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sijauliza urasimu huu unatokana na nini kuifanya nchi inadumaa kibiashara? Si hivyo tu Mkoa wa Mtwara, Mkoa wa Ruvuma tunapakana na nchi jirani zikiwemo Malawi, Zambia pamoja na Kongo DRC. Mizigo ya Kongo DRC imehama kutoka katika Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya urasimu, lakini tujiulize kwa nini kuwepo kwa urasimu wakati kuna eneo ambalo ni karibu Bandari ya Mtwara ambayo katika miaka ya nyuma ilikuwa inafanya kazi kubwa sana na ilikuwa inaheshimika kwa watu, ilikuwa iko busy, lakini kwa urasimu uliokuwepo Dar es Salaam, kwa sintofahamu iliyokuwepo Dar es Salaam wameifanya bandari ya Mtwara kuwa dormant. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ufuta unatoka Nanjilinji, ufuta unatoka Newala unakuja Dar es Salaam, lakini yote ni biashara tu kutaka kuleta mileage na kumkandamiza mkulima katika zao la korosho zao la ufuta, zao la kahawa zao la cocoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hayati Rais Mkapa alianzisha Mtwara Corridor kuhakikisha kuwa mazao yote ya Mkoa wa Katavi, Rukwa, Ruvuma, Mbeya, Lindi na Mtwara yote inatumia Bandari ya Mtwara. Kumetokea kidudu gani? Ameturoga nani mpaka kuifanya hii bandari isifanye kazi? Kutokana na urasimu, tunaona leo nchi zote za jirani zimekimbilia Beira Mozambique. Beira ukiiangalia inapakana na South Africa. Hivi jamani ifikie mahali tubadilike Watanzania, tusiendelee kulalamika. Tunahitaji mifumo ambayo watu wanataka kuileta Tanzania yenye maendeleo ili maendeleo haya yaonekane. Wenzetu wale waliokwenda kule, hawakwenda hivi hivi, kuna vitu tumewafanyia ambavyo havikuwafurahisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaona mkonge unatoka Tanga unapelekwa Dar es Salaam; kahawa ya Kilimanjaro inapelekwa Dar es Salaam; mazao ya Babati Mkoa wa Manyara yanapelekwa Dar es Salaam; Tanga iko wapi? Hivi leo tunazungumza Bandari ya Tanga haina mapato, siyo kwa kuwa haina mapato, Dar es Salaam pana ubadhirifu mkubwa, pana urasimu mkubwa mpaka umeifanya Bandari ya Dar es Salaam kuonekana kama ni bandari ambayo haina hadhi na heshima kwa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri wa Fedha akae na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, tujiulize maswali mengi, kwa nini inatokea hiyo hali? Tuna Kamati zetu za Bunge; Kamati ya Miundombinu, Kamati ya Bajeti, tuachane na masuala ya kukaa mezani, twende kwenye site. Unda tume itakayoonyesha kuwa inataka kuisaidia bandari. Leo bila kuwa na uchumi haiwezekani. Tunapata aibu kubwa, wenzetu wanatujadili katika Bunge letu, wanasikiliza maoni yetu, wanayafanyia kazi. Sisi tunakaa humu ndani tunaongea sana, tunatoa mawazo makubwa sana Wabunge, mawazo yetu hayafanyiwi kazi, matokeo yake ni urasimu. Urasimu huu umetufanya tuwe katika uchumi wa kati, lakini ilibidi tuwe katika uchumi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungukwa na nchi ambazo wakiitumia bandari hizi nyingine, tutatoka kiuchumi, lakini tuko wapi? Tunadhalilika, tunaaibika kwa ajili yetu wenyewe kwa sababu hatujipangi. Huwa nafika mahali najiuliza, hivi watendaji hawa wa bandari hawaoni bandari ya Mtwara kama ni bandari nzuri? Bandari ambayo ina kina? Nataka nijue kwa nini tunapata hasara na bandari? Mtwara tunakosa ajira kwa sababu hakuna kazi inayofanyika Mtwara. Ajira hamna. Tunakosa ajira Tanga; tungeifufua uchumi mkubwa sana katika mikoa hiyo miwili; Tanga na Mtwara na majirani zao wote wangeondoka kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka Mheshimiwa Waziri atakapotaka ku-wind aniambie kama majibu hayana maana nataka nichukue shilingi mnijibu hapa kuna nini? Wanasema sababu za msingi kwamba hakuna makasha. Hivi kweli tumebinafsisha section ya container terminal tumewapa TICTS, kwa nini TICTS anaing’ang’ania Dar es Salaam? Kama kazi imemshinda kwa nini asije kutuambia? Tunajikuta tumekaa, makontena yamefika pale yanatolewa, rushwa zote ziko katika Bandari ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda muafaka sasa hivi, tukitoka hapa tuwe na muda maalum maana yake hatuna time frame kuwa tukitoka hapa tuliangalie Bandari ya Mtwara, tuiangalie bandari ya Lindi na Kamati zote mbili hizi ziende katika eneo. Mimi sitoi amri maana amri anayo kiti, lakini naona kabisa tuko katika muflisi mkubwa na tukiendelea hivi wageni wetu wote majirani zetu watahama katika bandari hizi na uchumi wa bandari yetu utatokomea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi kwenye issue yangu ya pili ya viwanda. Tumevifunga viwanda kwa muda mrefu, hakuna maneno yanayozungumzwa humu ndani. Leo tunangojea kuletewa mafuta kutoka nje. Jiulize mbegu za pamba zinazolimwa katika mikoa ya kanda ya ziwa zinafanya kazi gani? Vile viwanda kwa nini mnavifunga mpaka leo? Kwa nini havifunguliwi? Tunajikuta tunaenda kukaa bandarini, kungojea mafuta kutoka nje, aibu hii kwa nchi hii itaisha lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mheshimiwa Mtaka ameonyesha uzalendo wa hali ya juu sana kutaka kufufua zao la Alizeti. Nami kama mwanamke na wanawake wote Tanzania nzima tumuunge mkono Mheshimiwa Mtaka, wanawake wote Tanzania nzima tulime angalau eka mbili za alizeti ili kuhakikisha aibu hii ya kuagizia mafuta nje itokomee kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka ni-declare interest, mimi mwenyewe ni mlimaji wa alizeti. Nalima alizeti, Lindi inastawi alizeti, tukitoka hapa ni kwenda Lindi kumuunga mkono Mheshimiwa Rais. Baada ya miaka miwili Tanzania hii hakuna tena kuagizia mafuta ya chakula kutoka nje. Mafuta ya chakula yatoke hapa hapa, kila Mbunge atoke hapa akiwa na neno moja; tunakwenda kulima Alizeti. Hakuna tena Mbunge kwenda kule, hapana; aonyeshe mfano; hawa Wabunge wote waonyeshe mfano, kila mmoja awe na eka tano tano katika eneo lake, alime Alizeti. Hii isiwe hoja ya Mheshimiwa Riziki, iwe hoja ya Kitaifa ili tukitoka hapa tuwe na legacy.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RUZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia hii nafasi.

Vilevile namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema, ambaye ametujalia kuwa na afya njema na kupata faraja, tunafurahi kama wenzetu wanavyozungumza humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa moyo wangu wote, napenda nimpongeze Mheshimiwa Rais, Mama mpambanaji ambaye ameamua kutupeleka mbele katika mapambano ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nawashukuru watendaji wote akiwemo Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Spika, Naibu Spika na Waziri wangu ambaye ni Mjumbe katika Kamati yetu ya Bajeti, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba. Huyu mimi namwita mpambanaji. Ninaamini kwa haya anayoyasikia humu ndani atayafanyia kazi ili utekelezaji wake uwe mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba ni Balozi wa Watu Wenye Ulemavu; anawapenda walemavu na ninapenda kumpelekea salamu zake kama walemavu wanasema wanakupenda, tena karibu sana, uwe nao karibu. Nao wana imani kuwa katika Mpango wako hautawaacha nyuma walemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia upande wa kilimo. Kilimo kinachangia uchumi wa shilingi trilioni 44, sawa na asilimia 26.9 ya pato kubwa la Taifa ambalo ni shilingi trilioni 163, lakini ukuaji wake ni 3%. Tujitafakari na tulitathmini, kwa kundi kubwa la asimilia 66 ya Watanzania, wanapata ajira na mapato yao kupitia kilimo. Katika ukuaji huu wa 3% mpaka 4% bado tuna changamoto kubwa katika eneo hili. Maeneo mengine ni ya watu wachache, lakini unapozungumza kilimo, unamzungumzia mkulima aliye kijijini, ambaye anategemea Bunge hili limkomboe na limtoe katika umasikini kumpeleka mbele. Kama uchumi tuna asilimia tatu, tunahitaji nguvu ya ziada katika eneo la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wote humu ni mashahidi, tunakwenda kukutana na changamoto za wanavijiji wakiwa katika hali ngumu na wanahitaji msaada wa kukombolewa. Niliongea katika Kamati ya Bajeti, tumepata pesa za Covid, lakini mkulima hayumo. Kama mkulima hayumo, ina maana siyo priority; lakini kwa vile ni mpango tunataka kuutekeleza hela nyingine zote zilizobakia tuzifanyie mpango tuone tunafanya nini ili kuingiza pesa katika bajeti ya kilimo ili iweze kumkomboa mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaizungumzia leo Novemba na Novemba tayari tunategemea mvua za vuli zinaingia na hatuna mbolea. Mbegu hakuna. Tusimame kwa Pamoja, hakuna haja ya kumwambia yule amekosea, amekosea, hapana. Watanzania twende kwa umoja wetu, tujue changamoto hii ya mbolea, ya pembejeo na mbegu tunalifanyia kazi. Tutume haraka kabisa, maana yake tukisema tunangojea muda fulani, suala hili linatakiwa maamuzi yake yawe ya haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia katika Mkutano Mkubwa wa Mabadiliko ya Tabia ya Nchi Duniani, mnaiyona kama ni rahisi sana. Tunazungumzia uchumi wa dunia unaozungumzwa katika nchi za Umoja wa Mataifa. Nimeangalia katika baadhi ya magazeti, nimeyasoma na ma-bulletin zimetolewa grant nyingi sana za kilimo. Kilimo wamekitangaza, small grant kwa ajili ya wakulima. Je, sisi Watanzania tuliokaa humu ndani, hatuna ripoti yeyote tunazopata kwa wenzetu wanapokwenda katika mikutao mikubwa kama hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matumaini yangu kutoka sasa hivi, wale wanaokwenda kutuwakilisha katika mkutano mkubwa wa Climate Change waje watupe mabadiliko ya tabia ya nchi na nini inabidi tufanye kwa Tanzania katika masuala ya kilimo, masuala ya afya na masuala mengineyo ambayo yanahitaji kubadilisha uchumi wetu kutoka hasi kwenda katika maeneo chanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata nafasi ya kutembelea bandari. Nilikuja na hoja ya Bandari ya Mtwara na Bandari ya Tanga. Tuipe kipaumbele. Nikupe taarifa, ninaona njia nyeupe ya kuleta mabadiliko ya bandari hizo mbili na pengine na bandari nyinginezo. Bandari ya Mtwara ni bandari ambayo ina uchumi mkubwa kama itasimamiwa wa nchi za jirani ikiwemo Zambia, Malawi na Congo na ndiyo maana ilianzishwa Mtwara Corrido kwa ajili ya kuhakikisha mazao yote katika Mtwara Corridor yanapelekwa Bandari ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza, Bandari ya Mtwara haina makasha. Hivyo watu wanatamani mizigo yao waipeleke Mtwara, makasha yako wapi? Hakuna. Nilitamani katika pesa ambazo zitaandaliwa, iwemo bajeti ya kupata makasha ili Bandari ya Mtwara ianze kufanya kazi. Tumekubaliana na Waziri Mkuu alitoa azimio kuwa korosho zote za Mtwara, Ruvuma (maana yake sasa hivi korosho mpaka Njombe kote wanalima, mpaka Mbeya wanalima) zipelekwe Mtwara. Imeshindikana, Mtwara hakuna makasha. Bado tunampa mkulima mzigo wa kuondoa mzigo wa Korosho kutoka Lindi au Mtwara kuupeleka Dar es Salaam.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu za kwanza ni kwamba, badala ya ile tozo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lulida kengele imeshagonga.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Aaah! Naunga mkono hoja na ninakushukuru sana.
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuunga mkono hoja ya kuumunga mkono Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli sina la kusema zaidi ya kusema Mwenyezi Mungu ni mkubwa. Mheshimiwa Rais ameonesha upendo mkubwa kwa watu wenye ulemavu. Hata hivyo, kitendo cha kuonesha upendo kwa watu wenye ulemavu, leo dunia inaitambua Tanzania iko katika ramani ya upendo kwa watu wenye ulemavu na walemavu sasa hivi wanasikika na wanaeleweka.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia maeneo ambayo Mheshimiwa Rais ameonesha. Alikula chakula na watu wenye ulemavu Ikulu na aliwapongeza kwa kazi kubwa waliyoifanya kwa kupigania Mchezo wa Mpira. Akiwakilishwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza alituletea Shilingi Milioni 150 kwa watu wenye ulemavu, wakasema hatutakuangusha, tuliweza kushinda mpira wa East Africa, tukashinda Mpira wa Afrika, tukaingia katika World Cup. Haya ni mafanikio ambayo hajaweza kufanikiwa Yanga wala Simba. Tunaomba nao wajitahidi kama walivyofanya walemavu. Natamani siku moja nisikie Simba au Yanga wameingia katika mipira mikubwa kama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kupitia huo mchezo, sasa hivi vijana 12 wameajiriwa nje ya nchi kama ma-professional Soccer, wanapata mahitaji yao na wengine wameniambia Mama cha kushukuru hatuna, tunatamani tukirudi kule turudi tena kwa Mheshimiwa Rais kumwambia tumefanikiwa kwa hili na sasa hivi familia zetu zinanufaika kwa ajira zetu nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi sina budi kwa hilo niseme tu Mwenyezi Mungu azidi kumbariki, azidi kuwapenda watu wenye ulemavu na vijana kwa ujumla na watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, kwa kupitia Wizara ya Madini, nimpongeze Mheshimiwa Rais mwamko huu na spirit aliyokuja nao baadhi ya Mawaziri wanaiga kuonesha spirit ya kuwapenda watu wenye ulemavu. Kwa kupitia Shirika la STAMICO tumepewa vitalu vya kuchimba dhahabu Mbogwe. Mimi mwenyewe nimekwenda pale kugawa vifaa kwa watu wenye ulemavu wenye usikivu hafifu, leo walemavu wanachimba dhahabu. Je, haya sio mafanikio? Tutanyamaza vipi bila kumpongeza kwa kuona leo walemavu wanataka kuuza dhahabu kwa kujifanya na wao wataondoa umaskini? Naomba na Wizara nyingine na taasisi nyingine ziige kama zilivyofanya Wizara ya Madini na STAMICO.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Wizara ya Kilimo kwa kupitia mfumo huu waliokwenda na wenzao, wao wametoa hekari 50 kwa baadhi ya wilaya kuhakikisha walemavu wenye ulemavu wa ngozi wanaanza kulima. Kwa mfano, Chamwino wametoa hekari 50 kwa watu wenye ulemavu na taasisi ya ASA ikishirikisha na mwenyewe Bashe aliwaambia wapeni mbegu, wakapewa mbegu za alizeti na mbegu za mahindi. Huu ni mfano wa kuanza nao kuhakikisha na maeneo mengine wanatoa ardhi kwa watu wenye ulemavu walime. Kwa vile walemavu sio wote ambao hawawezi kulima, walemavu wenye usikivu mdogo wanaweza kulima, walemavu wenye matatizo ya ngozi wanaweza kulima.

Mheshimiwa Spika, sasa hii speed ya Mheshimiwa Rais twende nayo vizuri ili angalau tunachosema sasa hivi kuwa haki ya walemavu katika maendeleo inclusion yanakwenda sambamba na speed ya Mheshimiwa Rais. Mwenyezi Mungu amzidishie zaidi Mheshimiwa Rais na walemavu wanasema wana neno lao kuwa wao wako pamoja na yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, CRDB Bank ikishirikiana na waendesha bajaji 500 wa Jiji la Dar es Salaam, wameamua kwa pamoja kushirikiana nao kwa kufungua akaunti ili walemavu wale wasinyanyasike. Wanachukua mikopo huku mitaani ya shilingi milioni 14 kwa wahuni huko mitaani matokeo yake wanashindwa kurudisha pesa, wanakuwa wanatumika visivyo. Hata hivyo CRDB Bank kwa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais, kwa kweli ni lazima tuyapongeze haya mashirika ambayo yako karibu na watu wenye ulemavu na tayari tunaona kabisa kama watu wale watawakomboa walemavu ambao wanahitaji mahitaji maalum.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge, wakafanye kazi ya kupambana kule chini. Hakuna wa kuachwa nyuma nobody should be left behind there is nothing about us without us. Walemavu wanahitaji inclusion katika kila eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, kwa speed hii tunayokwenda nayo Mama ameongea neno moja zito kwa Watanzania amesema, tuwe mabalozi twende tukawalinde vijana wetu kule chini, wasiige tabia na utamaduni ambao sio wa kwetu. Kwa vile Tanzania ni Nchi huru ina sheria zake, taratibu zake, Dini zake, lakini vile vile ina mila na desturi. Hivyo wasituletee mila ambazo zitakuja kuwafanya watoto wetu wawe dhaifu kwa ajili ya wanachokitaka wao hapana.

Mheshimiwa Spika, hili neno limewafanya Watanzania wamekosheka, kuwa na faraja kuwa watoto wetu ambao wanataka kuharibiwa kila mmoja akawe balozi katika eneo lake. i Wabunge katika kila…

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika, naomba pia nimkumbushe Mheshimiwa Riziki kwamba Mheshimiwa Rais mwaka 2022 ametoa shilingi milioni 60 kwa ajili ya mafuta ya watu wenye Ualbino na hii iko kwenye mchakato wa Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwa hiyo, ninachotaka kumkumbusha kwamba Mheshimiwa Rais anafanya mengi sana ambayo tutaweza kila siku kuyasemea na kuyatetea na kuyapigania. Kwa namna hiyo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Riziki Lulida unaipokea taarifa hiyo?

MHE. RIZIKI S LULIDA: Mheshimiwa Spika, hiyo taarifa ni lazima niipokee, ni taarifa yenye mafanikio na ni kweli wenzetu wenye matatizo yaN wamepewa Mafuta ya Mabilioni. Sasa hivi tunae balozi wetu ambaye ni Mheshimiwa Mwigulu Nchemba amesimama na watu wenye ulemavu kuhakikisha hela zao za mikopo zinapatikana. Vile vile, Mheshimiwa Mwigulu ni balozi wa watu wenye ulemavu napenda awe pamoja na watu wenye ulemavu ili aweze kufanya nao kazi kwa pamoja ili walemavu hao wasihangaike kuombaomba. Hakuna wa kuombaomba kila mmoja atakuwa pamoja na sisi, tufanye kazi kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema tena naunga mkono hoja hii kwa kusisitiza Mheshimiwa Rais kwa kweli anafanya kazi kubwa kwa kupitia vijana na watu wenye ulemavu. Nasema ahsante na Mungu azidi kumbariki, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kutujalia afya njema na kuwepo hapa. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa Hotuba nzuri ambayo ametuletea hapa, tuzidi kumwombea Mwenyezi Mungu, amjalie aweze kufanya kazi kwa njia akiwa na afya njema na atubariki sana tumepata bahati nzuri kuwa na Waziri Mkuu msikivu, mpole, mwenye hekima, ana uwezo mkubwa, Mwenyezi Mungu mbariki zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nipo hapa kumshukuru sana sana Mheshimiwa Rais wangu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan, ni mwanamke jasiri ambaye ana upendo kwa kila kona anaonyesha nini anachokifanya na mimi nitazungumza kwa yale ninayoyaona kwa macho yangu kama ushuhuda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania asilimia 67 ni vijana na hawa vijana ni kundi kubwa ambalo inabidi lifanyiwe kazi ili kuweza kuleta uchumi wa nchi. Leo tunaona vijana wanamaliza vyuo vikuu, wanamaliza katika maeneo mbalimbali lakini hawana ajira na Wizara tuliyokuwa nayo hii sasa ya Wizara ya Vijana, Kazi na Maendeleo ya Jamii kuna hitaji msukumo mkubwa sana wa kuhakikisha kuwawezesha hawa vijana baadaye usije ukawa mzigo wa nchi. Nitazungumza kwa ninayoyafahamu, leo hili vijana hawa waweze kupata ajira, wajiajiri wenyewe, Serikali ni lazima ihakikishe inawapelekea fedha na inapeleka fedha kwa wakati ili waweze kusomeshwa na wajiajiri wenyewe baadhi ili kuweza kusukuma uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilikuwa katika mkutano wa madini. Tumeambiwa wachimbaji wadogo wadogo ambao ni vijana na wanawake wameweza kuleta pato la Taifa asilimia 40 vis-a-vis wawekezaji wakubwa lakini changamoto waliyokuwa nayo wale wanasema hawana mitaji, hawana vitendea kazi. Sasa kama hawa wanaweza kuleta pato la uchumi mkubwa kwa asilimia 40, unayaachaje makundi haya yasiwezeshwe? Tunakwenda katika bajeti kuna SGL ambayo inabidi iende asilimia 30 iende kwa vijana, walemavu, wanawake lakini nimeshangaa imepelekwa bilioni tisa badala ya bilioni 87.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukajaribu kujadiliana wakasema baadhi ya pesa hizi zinakwenda kwa mifuko (mkopo) board loan, sawa, lakini haiwezekani bilioni 87 zote wapeleke katika mikopo ya wanafunzi, wanaliacha hili kundi kubwa ambalo linaingia mtaani, halina kazi, halina mtaji, wanategemea kuzalisha kitu gani? China, India, Singapore, Malaysia walisimama na vijana na walihakikisha wanasoma katika vocational training centers ili badaye waje waweze kujitegemea wao wenyewe kwa kuweza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaambiwa katika eneo hili hapatengwi pesa ya kutosha, wanasema hawaweki pesa, kama huweki pesa unategemea hili kundi wanalipeweka wapi? Hili kundi litatuletea zogo baadaye maana yake vijana wakikaa baadaye akijiona amemaliza PhD, sina kazi, si ajiriwi, watu wanaajiriwa kwa mafungu ambayo ni ya watu wachache, makundi maalum, hawa vijana ni lazima, naomba hizi pesa tulikubaliana juzi na Waziri wa Fedha, atakuwa shahidi walisema watakwenda kukaa, nataka waje watuambie hapa wametenga kiasi gani angalau basi watupe robo. Katika bilioni 87 wakitupa robo angalau kundi hili la watu 42,000 ambao tumepanga waanze kupata mafunzo liweze kufanya kazi. Si hivyo tunawapa mzigo mkubwa Wizara ya Kazi na Vijana wakati hawana kazi ya kufanya nao na tutahakikisha vijana hawa badala ya kupata mafunzo maalum, itakuwa vijana hawa ni vibaka, ombaomba mitaani na tutaendekeza wengine wajiingize katika masuala ya ushoga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetembelea maeneo mbalimbali, tumekwenda Tengeru Meru. Vijana wana degree zao wameamua kutengeneza greenhouse zao, wale vijana sasa hivi wanauza mboga, wanauza matunda, wanapeleka maua nje ya nchi. Matokeo hayo ni kwa sababu wamepewa incentive, tujifunze Halmashauri ya Meru nini wamefanya kuwasaidia wale vijana ili halmashauri zingine Tanzania nzima wajifunze ili kuhakikisha vijana waliopo kule wanapata mafunzo na wanapewa greenhouses ili wawatoe katika umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi maalum la watu wenye ulemavu; toka mwaka 2015 tunazungumza mpaka leo hawajaweka bajeti hata senti tano katika Kifungu cha Vijana na Mikopo. Leo walemavu nina PhD za walevu zaidi ya sitini hawana ajira, nina masters za walemavu hawana ajira, nina degree za walemavu hawana ajira, basi hata fungu lao la hela hawawekewi allocation ya funds hata kidogo. Walisema watatupa bilioni tatu, mpaka leo napata kigugumizi kusema kuwa hata senti tano haijawekwa. Mimi ni mlengwa, ni mlemavu niliyepata ulemavu nikiwa hapa Bungeni, naona maumivu makubwa ambao wanapata watu wenye ulemavu katika kuwa kwanza hawaajiriwi, wanawaona kama siyo haki yao ya kuajiriwa, lakini hata hii mikopo yao ya kuwasaidia hili waweze kujiendesha wenyewe nayo ni kigugumizi. Hii ni Wizara na hii kama ni Wizara wote watu wa Wizara wananisikiliza, hili kundi maalum la watu wenye ulemavu na hizi bilioni tano ambazo Waziri wa Fedha alisema atazitoa, naomba zifanye kazi na zitolewe ili hawa watu isije ikawa baadaye ni mzigo na kulaumiwa wanaitwa ombaomba sijui maskini, lakini si maskini hawa wana akili tosha na wana uwezo tosha wa kufanya kazi. Mfano Mbogwe, STAMICO tena Wizara ya Madini inasimama na watu wenye ulemavu wamewapa vitalu, wanachimba dhahabu, kwa maana moja hata mlemavu ukimwezesha anaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia barabara Mkoa wa Lindi, ni toka tumepata Uhuru na Waziri Mkuu wa Kwanza wa Tanzania hii alikuwa Mheshimiwa Rashid Mfaume Kawawa, anatoka Liwale. Barabara ya kutoka Nangurukulu mpaka Liwale mpaka leo ni kigugumizi, hakuna jibu linalotolewa na Serikali, tumedanganywa sana kuhusu barabara ya Liwale, barabara hiyo ya Liwale hata kumuenzi Mheshimiwa Rashid Mfaume Kawawa, ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa Nchi hii. Barabara ile haitengewi, watu wa Liwale leo wanakwenda huko kwa siku mbili anatoka hapa anakwenda mpaka Lindi, Lindi Nachingwea, Nachingwea anakwenda mpaka Liwale. Naomba nipate majibu kwa nini Barabara ya Lindi ya Nangurukuru – Liwale mpaka Nachingwea imekuwa kigugumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nitazungumzia masuala ya kijinsia. Ukisikia neno demokrasia ndani kuna jinsia, Tanzania ni Nchi huru, Tanzania tuna utamaduni wetu, Tanzania tuna culture yetu sasa hatutaki kuingizwa katika mambo ambayo wao wanayataka kwa ufirauni wao ili kutuletea Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kitabu cha Quran nitazungumza kwanza huko, wanasema “Walaa taqrabu zinaa, innahu kana faahishatan wa saa sabiila” akasema tena “Azaniyatu wazanii fajilidu kulla wahda miatu-l-jadda” hakika vitabu vyote Biblia na Quran vinakataza zinaa, lakini siyo zinaa tu, ikija huko ndiyo hatari kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitaje miji ambayo ni hitarishi sasa hivi ambayo inaangamia kwa ajili ya ushoga. Kwanza Zanzibar, watalii wanaokwenda Zanzibar wako huru wanakuja wanaume kwa wanaume, wanalala mahotelini, tunataka Zanzibar ionyeshe mfano. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Riziki Lulida, ahsante sana.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kunijalia na kutujalia sisi sote tukiweo hapa afya njema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamo wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Waziri wa Madini na Watendaji wa Wizara ya Madini. Mheshimiwa Rais tarehe 17 aliweka Saini mkataba mkubwa wa dola milioni 667. Mkataba huu unakwenda kuleta uchumi mkubwa katika Mikoa ya Lindi, Songwe na Mkoa wa Morogoro. Mikoa hii kwa muda mrefu ilikuwa inasemekana kwamba ina madini ya kutosha lakini ilikuwa bado kigugumizi. Sasa, kitendo cha Mheshimiwa Rais kufungua na kuingia katika mikataba rasmi kwa kweli tunaona kabisa Lindi kuchele. Naona Ruangwa kuna dhahabu, graphite na madini madogo madogo. Tunaona Liwale kuna dhahabu lakini ndani ya Selous kuna wachimbaji, ambayo tunaona wanachimba kiholela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matumaini yangu kuwa Serikali itakuwa macho, wale waliopewa vitalu kule ndani wasitufanye shamba la bibi, tunataka tuhakikishe yanayopatikana ndani ya Selous au yale madini kama kuna wachimbaji wanajificha ficha, hasa watu wenye sura pana; nilipata nafasi mimi ya kuzungukia na nilipewa muda na watu wangu wa Habari Conservation, wa kutembelea maeneo ya corridor ya Wanyama tukakuta maeneo watu wanachimba, lakini financer wakubwa ni sura pana. Sitaki kutaja majina watasema Riziki umetaja mananii ya watu lakini tafuteni ni na sura pana wanajulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 nikiwa Kamati ya PIC nilikuja na recommendation kuwa STAMICO ifutwe kabisa imeingia katika hasara ya nchi, lakini hawa STAMICO walikuwa wameingia katika hasara ya nchi kwa ajili ya mikataba ambayo wao haikuwahusu. Ilikuwa ni mikataba midogo ambayo imeifanya STAMICO wawe paralyzed; lakini leo nataka nitoe ushahuda wangu mwenyewe STAMICO inakwenda juu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 STAMICO imeweza kupeleka gawio la Serikali bilioni 2.5, na mwaka huu tunategemea kupata bilioni tano kwa taasisi ambayo ilishakufa haikuwa na mishahara na haikuwa na uwezo wowote. Lakini, kwa kupitia Mkurugenzi Mkuu, kwa uwezo aliokuwa nao wakishirikiana na watendaji wa STAMICO sasa STAMICO ni taasisi moja wapo inayoongoza, na inafanya kazi kubwa ya kuleta Tato la Taifa. Hongera sana Mkurugenzi Mkuu Venant Mwase, endelea kufanya kazi, Watanzania tuna matumaini makubwa na wewe. Sasa hivi nenda Lindi kahakikishe kila kanda wanafanya competition ya kujua yako wapi madini ili watu wa pale waweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa kamati ya LAAC mwaka 2007 nikatembelea Geita. Ilikuwa kwamba katika mikoa sita maskini na Geita mojawapo, leo nimeenda Geita nakuta mpaka traffic lights ziko barabarani. Nimetoka Geita, Katoro mpaka Bwanga watu wa kule sasa hivi unaona kabisa maisha yao mazuri. Niwapongeze Rais wa Madini Mr. Bina hongera sana kwa kazi kubwa unayoifanya kuwasimamia wachimbaji wadogo wadogo, ambao nao sasa wananufaika. Nimpongeze mwanamke shujaa Semeni John, huyu ni mwenyekiti wa wanawake wa wachimbaji wadogo wadogo. Tulikuwa kwenye mkutano mkubwa sana wa wachimbaji wadogo wadogo, kwakweli ule mkutano umetufanya tufarijike sana. Wanawake, vijana na wenye ulemavu ndio wanaoingiza forty percent ya uchumi mkubwa wa dhahabu; lakini hawana vitendea kazi, hawana mitaji; ni kundi ambalo linachimba katika mazingira magumu. Huko ndiko Serikali inapaswa ipambane na isimamie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri tulikuwa naye anafanya kazi kubwa sana kuhakikisha tasnia hii inakwenda vizuri. Hongera sana Doto Biteko, mtoto msikivu, mwenye heshima, Mwenyezi Mungu azidi kukubariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninazungumzia sekta ya chumvi. Mikoa ya Lindi, Mtwara, Dar es Salaam, Pwani yote mpaka Tanga ni mikoa ambayo ilikuwa kando kando ya Bahari inashughulika zao la chumvi; hili zao lilikufa kabisa. Leo STAMICO wameamua kulifufua hili zao la chumvi kwa kutengeneza data ya kuhakikisha kwamba wanawajua wachimbaji wote wanafanya kazi gani ili kuweza kuingia katika soko la Afrika na SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chumvi inahitajika Rwanda, Malawi, Zambia mpaka Congo pamoja na Uganda. Kwa kweli akisimamia hili eneo na wananchi hawa wakanufaika na uchimbaji wao wa chumvi kwa kweli suala la umaskini Mikoa hii ya Kanda ya Pwani itakuwa imepungua; nimpongeze sana kwa kazi anayofanya. Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, anafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuja katika wachimbaji wadogo wadogo walemavu. Mimi ni shuhuda nilikwenda Mbogwe nikishirikiana na madini kwenda kugawa vifaa na mitambo kwa walemavu viziwi, wenye usikivu hafifu. Kumbe walemavu hawa mkiwatengea mazingira mazuri wanaweza kuleta uchumi mkubwa sana. Ningeomba baadhi ya Wizara zingine ziige mifano hii. Vile vile ningetamani mifumo iongee. Katika Wizara ya Wanawake tujue kuna wanawake wangapi wanachimba madini, hiyo naipa kazi Wizara; waje hapa watuambie wanawake hawa wanachimba madini. Lakini vile vile Wizara ya kazi wajue vijana wangapi wanafanya kazi ya kuchimba madini ili mafunzo yazidi kuendelea. Ninashukuru Waziri wa Fedha tayari ametoa bilioni tatu kwa ajili ya mafunzo kwa vijana. Hizi zikitumika kuwasomesha na kuwapa mafunzo maalum ninaimani baada ya miaka tunazungumzia utajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini ushauri wangu? Tuna kanda ya kati ina madini, kanda ya kusini ina madini, kanda ya kaskazini tumeona Mererani kote kuna madini angalau kule kumeshapewa mwelekeo mkubwa. Matumaini yangu kwa sasa hivi Serikali iangalie, mikoa hii ambayo ina madini kwa wingi haya madini yote yanakwenda panya road, na katika kwenda panya road hatuoni manufaa ndio maana kama sasa hivi unaona only forty percent inakwenda kwa wachimbaji ambao wanaonekana wadogo wadogo. Ina maana madini mengi yanayotoka hapa yanaingia katika panya road yanaingia katika utoroshaji kwenda nje. Sisi wenyewe tukiwa tunategemea kuwa na matumaini makubwa sasa hivi tupambane nyumbani kwanza, mzalendo kwanza, Mtanzania kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wengine wanakuja misamaha ya kodi, misamaha ya mafuta yote wapewe, misamaha ya mitambo, inakuwaje wanashindana na watu ambao wanatumia vingondoli na majembe wakawa wanafika forty percent? Hawa wachimbaji wadogowadogo wakiongozwa na akina John Bina, kina Semeni ninaamini kuwa watu hawa watatoka vizuri na wataweza kufanikiwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali, na nishukuru sana Serikali, Mheshimiwa Rais katika mradi huu ambao umekwenda Mikoa hiyo, hasa mimi Lindi, nasema ninamuunga mkono kwa asilimia mia moja. Ninakwenda Lindi kusimamia wachimbaji wadogo wadogo. Wanawake na vijana sasa hivi ni muda mwafaka wa kuwaingizia uchumi. Hii tunayopata sasa hivi mwakani tutegemee kupata maradufu. Mheshimiwa Waziri nipe nguvu, niko tayari kama balozi wako kusimamia hili na wala sitakuangusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti,baada ya kusema hapa ninawashukuru sana na ahsanteni sana; Mungu Ibariki Tanzania.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia sisi wote Afya njema tuko hapa kwa kuisaidia Serikali yetu chini ya Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, mwana mama shupavu ambaye ana nia nzuri ya kuhakikisha uchumi wa nchi yetu unakimbia. Nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya, Naibu Waziri na Katibu Mkuu na Watendaji wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado nina hoja yangu ya viwanda vilivyobinafsishwa. Mwalimu Nyerere alivitengeneza viwanda hivi kwa kanda maalum, na alihakikisha kila kanda uchumi wa kikanda unakwenda vizuri. Mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani tulikuwa na viwanda vya korosho 13. Viwanda vyote vimebinafsishwa na waliobinafsishiwa wamekaa navyo kwapani, hakuna wa kuwauliza wala wa kuwahoji. Wananchi wa Mikoa hii hawana ajira, na matokeo yake sasa hivi akina mama na vijana wameamua kutafuta vijimtaji vidogo vidogo, ndiyo vinaitwa viwanda vidogo vidogo, wanabangua korosho. Hii imetokana na bei ya korosho kuwalalia vile vile wale ambao wamechukua viwanda vile, ndio wanaonunua korosho kupeleka nje. Maana yake ni kuwa, uchumi wa Tanzania unachezewa na wafanyabiashara wakubwa wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na viwanda Mkoa wa Tanga; Viwanda vya Gossage, viwanda vya chuma, viwanda vingi vya kutengeneza mpaka biscuit Tanga, leo biscuit tunaagiza kutoka nje, pipi tunaagiza kutoka nje. Halafu mnasema Tanzania tunataka tuondoke na kuendelea katika uchumi wa kimaendeleo wa viwanda, ni pagumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi inaangamia sasa hivi kwa kuletewa vyakula vibovu. Tunaona katika mitandao, chocolate inafunguliwa imewekwa dawa ndani. Hizi dawa ni za kuwaangamiza vijana wapate hormones mbaya na zile hormones zitawafanya kuwa mashoga, na wakiwa mashoga watakuwa hawawezi kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona pipi, biscuit, juice mpaka maji na mafuta ya kula, lakini leo unashangaa kibali kinapita cha kuingiza mafuta tones of tones, lakini viwanda vyetu vyote vimefungwa. Nenda Shinyanga, tulikuwa tunakula mafuta mazuri ya Okay. Tulikuwa tunakula Super Ghee Tanzania, tulikuwa tunakula Tan Bond na tumepeleka mpaka nchi za Jirani. Ziko wapi Tan Bond? Iko wapi Super Ghee? Iko wapi Okay? Matokeo yake tunaagiza mafuta kutoka nje, haiingia akilini kwa Watanzania kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanakosa ajira ya viwanda vyao, tunawaachia wafanyabiashara ambao wanasema wamewekeza, halafu vitu vyote, leo material zinapelekwa nje, wanatuletea mafuta machafu ambayo yanabadilisha afya za Watanzania. Hii haikubaliki. Kwa kweli inabidi tusage meno na tutafute mazingira magumu ya kuikwamua nchi. Pipi inatoka India, chocolate inatoka China, juice zilizoharibika viwandani, zilizo-expire wanazibadilisha dating wanazileta Tanzania. Jamani tunawahurumia watoto hawa? Tunaiuhurumia nchi? Mimi leo lazima niseme ukweli maana yake napita kujiuliza kwa miaka yote 20 tunazungumza neno hili hili, lazima lifike mwisho. Hili neno la kuagiza kila kitu kutoka nje, mpaka toothpick inatoka nje, lazima ifike mwisho. Jamani, enough is enough.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile viwanda vilivyofungwa, Wabunge ninyi nyote tuungane kwa pamoja tumsaidie Mheshimiwa Rais. Rais anafanya kazi, sisi tunafanya nini humu ndani? Kazi tuliyokuwanayo ni moja, tumuunge mkono kwa kuhakikisha tunaazimia kwa pamoja, tuiombe Serikali walete taarifa katika Kamati ya Viwanda na Biashara, wawekezaji wote ambao wamewekeza sugu na viwanda havifanyi kazi na wamekaa navyo na baadaye havifanyi kazi na kuhakikisha ajira hamna, kuwa tunawaonea aibu, aibu gani wakati wote ni matajiri. Tunashindwa kutoa ajira! Nenda Mkoa wa Lindi, aibu tupu! Hatuna kiwanda hata kimoja. Tunategemea kiwanda cha korosho, nacho kimefungwa. Aliyefunga nani? Mimi na wewe hatujui. Kwa nini tufikie hapo? Kwa nini tumwache mwananchi wa Nangaro hana kazi? Kwa nini tuwafanye akina mama na vijana hawana kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna vijana ndekejo ambao wanahangaika hapa wamemaliza vyuo vikuu hawana kazi, viwanda vimefungwa; na mtu aliyevifunga anakuwa na ubavu wa kusema hakuna wa kuniambia nifungue kiwanda hiki. Kweli nchi hii ya kweli ilimkomboa Mwafrika na Mtanzania kweli! Ni ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, azimio langu, au ushauri wangu, Serikali sikivu itumie TR kuhakikisha anapeleka katika Kamati taarifa yote ya viwanda vyote vilivyofungwa ili wajulikane kwa nini wanaleta kiburi hiki? Pia alipe faini, maana yake haiwezi kuacha kwa kumhoji tu, amekaa miaka mingi, miaka nenda miaka rudi hakifanyi kazi, na ametumia nafasi hiyo kuchukua mikopo benki, lakini wanachi hawana ajira. Hivi vitu lazima tukubali kwa pamoja. Tuungane Wabunge wote kwa pamoja tuwe na azimio moja la kuhakikisha viwanda vinafunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa ya Pwani tunatengeneza chumvi, tuna viwanda vya chumvi. Lindi chumvi, Mtwara chumvi, Tanga Chumvi, na Pwani chumvi. Amekuja mwekezaji, anawekeza kiwanda cha chumvi, analeta chumvi kutoka India. Mheshimiwa Rais mpendwa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan alikuja Lindi, akasema, ninajua kero ya Lindi ni chumvi. Naomba ufumbuzi upatikane. Mpaka leo, chumvi inaletwa kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo watu wa Lindi wamekaa na chumvi, watu wa Mtwara wamekaa na Chumvi. Uchumi wa Pwani ni chumvi. Leo chumvi inatoka India mpaka inafika Tanzania, inaachwa chumvi kutoka Kilwa tones of tones, watu wamechukua mikopo mpaka wame-paralyze, wanauziwa majumba yao, lakini chumvi zimewajalia majumbani, hakuna mahali pa kupeleka, eti kisa, mwekezaji ametafuta soko la Tanzania na kuhakikisha anatumia soko la Tanzania kupeleka chumvi Burundi, kupeleka chumvi Rwanda, kupeleka chumvi Zambia, kupeleka chumvi Uganda. Sisi wetu Watanzania masikini, watu wa chini wanahangaika na chumvi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na Mkutano wa Madini, nikaenda pale, wananchi wanasema je, mikopo hii mtaifanyaje? Tumechukua mamilioni ya mikopo benki. Benki, wao wanaweka riba tu, na riba ikifizidi wanauza nyumba yako. Chumvi iko ndani. Hili siyo la kuliachia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbunge wa Mwanza analia, Mbunge wa Tanga analia, Mbunge wa Kagera analia, sasa tunakwenda wapi? Hatuna maamuzi. Bunge hili liwe strong, Bunge la kufanya kazi lililotuleta hapa, tumkomboe mwananchi. Mwananchi huyu ndiye aliyetufanya sisi hapa tukaitwa Wabunge. Kama tutakuja hapa hatujawasaidia wananchi wale, kwa kweli tumehangaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la mwisho. Mimi natoka Lindi, nataka nipate majibu, Kiwanda cha Korosho cha Lindi, maana yake kwanza ndiyo eneo la kujidai, kinafunguliwa Lini? Kiwanda cha Tandahimba kinafunguliwa lini? Majibu hayo yawe na muda, siyo nikae hapa mpaka mwaka mzima, kesho tena nianze na biashara hii, siwezi nikakubali. Kwa kweli inanikirihisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dharau tunavyodharaulika watu wa kusini kuonekana masikini, hatuna viwanda. Viwanda vile vilikuwa vinaajiri watu 3,000, leo hakuna hata mtu mmoja, vimefungwa, mashine zote zimetolewa. Kama mnabisha hapa, tuondoke twende Lindi tukafungue viwanda mwone kama mtakuta mashine ndani ya vile viwanda. Wame vinyofoa na hakuna wakumwuliza chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipatia hii nafasi. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu Waziri Mheshimiwa Chande, lakini vilevile nitoe shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya na kuhakikisha ile miradi ambayo endelevu ya kutoka Awamu ya Tano kwenda katika Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya. Tunamwona muda wote yuko mbioni akihakikisha kuwa maeneo mbalimbali ambayo yana utata, yeye anakwenda kuyarekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitaishukuru sana Serikali kwa ajili ya Mkoa wangu wa Lindi. Mkoa wa Lindi ni mkoa Tajiri, lakini ulikuwa nyuma hasa katika maendeleo kwa vile ulikuwa hauna miradi. Sasa nitaitaja miradi ambayo ni mikubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameipitisha katika mwaka huu. Mradi wa kwanza umesainiwa Mradi wa LNG, huu mradi ni mkubwa ambao unakwenda katika eneo la Likong’o katika Jimbo au Manispaa ya Lindi. Utaleta mafanikio makubwa katika nchi yetu, lakini ningeomba sana katika huu mradi Wabunge tuje tupewe taarifa nini kinaendelea katika LNG? Mafanikio ya LNG, lakini vilevile tunataka wananchi wetu kule wajue wanatuuliza maswali mengi ili kujua nini kinaendelea katika LNG? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Waziri mwenye dhamana aje afanye semina na Wabunge, aende Lindi na Mkoa wa Lindi na Mtwara tuunganike tujue lini LNG inafanyika? Maendeleo yale yawazindue wananchi ili wajitambue katika suala la local content na miradi ya corporate social responsibility ili na wananchi wajiandae kibiashara kwenda na maeneo hayo. Tunahitaji mahitaji ya smart city kwa ajili ya wale wanaokuja kuwekeza wasije kwenda mikoa ya jirani kwa vile Lindi hatuna mahoteli ya kutosha. Tunaomba uwekezaji mkubwa wa mahoteli na maeneo mbalimbali katika Mkoa wa Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi mkubwa vilevile ambao umezinduliwa mwaka huu Ikulu, Mradi wa Madini ya Graphite Ruangwa – Chilola. Huu ni mradi mkubwa na Lindi ambayo ilikuwa ya maskini, itakuwa ni Lindi ya matajiri. Ni mkoa ambao una ufanisi mkubwa katika madini. Ni matumaini yangu Wanalindi tumefika muda sasa hivi kuwa tumuunge mkono Mheshimiwa Rais, anafanya kazi kubwa sana kuhakikisha hatutakuwa tena ni mikoa maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa tatu, miaka nenda tulikuwa tunalia barabara Nangurukuru, Liwale, Masasi, mwaka huu wameshasaini tayari barabara ya lami na nina imani itatoa kero na uzia mkubwa na ambao tulikuwa nao kwa ajili ya barabara hizi ambazo zilikuwa hazipitiki. Ilikuwa Mbunge wa Liwale kipindi cha masika hawezi kwenda Liwale, lakini huu ukombozi wa kutupatia huo mradi mkubwa wa kupitisha barabara nasema Mwenyezi Mungu azidi kumbariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati juzi tulitembelea Arusha, tumepata taarifa kutoka kwa Mkuu wa Mkoa Royal Tour imeleta mafanikio makubwa sana. Watalii wamejaa Arusha ila tuna changamoto hatuna hoteli. Tunaomba wawekezaji wakubwa, tunahitaji uwekezaji, hakuna kupinga uwekezaji. Uwekezaji uliokuwa umetukuka na mikataba mizuri ijenge mahoteli, hii Royal Tour ambayo tumeleta watalii wengi wapate mahali pa kukaa na kuweza kujisikia raha katika utalii wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwaombe TANAPA wajenge mahoteli, tuwaombe Ngorongoro wajenge mahoteli, wachukue mikopo wajenge hoteli kwa sababu sasa hivi watalii wanahangaika, wanakwenda kulala katika mahoteli ya chini kabisa na kwa kweli Arusha imefurika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji wa Bandari; sisi tunahitaji uwekezaji. Mikoa ambayo inazungukwa na bandari tunahitaji ufanisi mkubwa sana katika uwekezaji. Hizi changamoto wanazolalamikia wananchi kama sheria mbalimbali zifanyiwe marekebisho na ni matumaini yangu ushirikishwaji wa bandari na uwekezaji umeshirikisha Bunge, umeshirikisha Mashirika ya Dini, Waziri Mkuu vilevile amekwenda kutoa ufafanuzi, sijawahi kuona eneo ambalo limeingia mradi limeshirikisha wananchi kama mradi huu. Nini faida yake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, faida ya kwanza SGR itafanya kazi, tutakuwa na mzigo wa kutosha ambapo reli hii tunayotengeneza itapata mzigo hapa kupitia huu Mradi wa Bandari. La pili, TAZARA ambayo imekuwa haina mzigo, mizigo itakayokuwa inakwenda Zambia itakuwa inapita katika reli ya TAZARA. Ni kitu ambacho ni kizuri, lakini kwa nini watu wanapiga kelele? Kuna maeneo matatu yana changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu ambao ni competitor, hawakubaliani na huu mradi hata siku moja. Competitors kwa vile mizigo mingi ilikuwa inakwenda nchi za Jirani, hawatakubali Tanzania iweze kupata mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mawakala, kuna mawakala wamo mle ndani ambao walikuwa wanafanya biashara ya kupitisha mizigo bila kufuata sheria. Anasema mzigo huu ni wa transit, anapiga mihuri humu njiani mote, lakini mzigo uko Dar es Salaam. Wale wanaona kabisa katika kuleta ufanisi huu, katika uwekezaji na wao watapata changamoto na ulaji wao utakuwa haufanikiwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira katika bandari zetu za Mtwara na Tanga. Mkoa wa Mtwara ile bandari ilishasimama kwa muda mrefu. Ni imani yangu uwekezaji huu, utafufua uchumi katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma. Mzigo ambao unatoka Zambia, unaotoka Malawi, badala ya kuja Dar es Salaam utakatisha Makambako kuja Lindi, kuja Mtwara. Kwa kweli sisi hatuna cha kusema zaidi ya kusema, yale ambayo yanatakiwa kufanyiwa marekebisho yafanyiwe marekebisho na ni imani yangu kuwa Mheshimiwa Rais anawapenda wanawake, anawapenda Watanzania, hathubutu kufanya kitu ambacho hakitaweza kumfanya yeye apate nanii, mama ni mlezi, wakati wote mwanamke ni mlezi, hawezi mwanamke mwenye ulezi wake akataka kuiangamiza. Huu mradi naomba Mwenyezi Mungu ausimamie na katika kuusimamia kwake, Watanzania tutakuja kufarijika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nasema naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nimuunge mkono Mheshimiwa Waziri, yeye ni Balozi wa watu wenye ulemavu, ametoa bilioni 1.0 kwa ajili ya kusaidia watu wenye ulemavu na kutuwekea Mfuko watu wenye ulemavu. Walemavu wanasema yeye ni Balozi wao na hawatamwangusha, tuna kila namna ya kusema ahsante kwa niaba ya walemavu wote Tanzania, nasema Mwenyezi Mungu azidi kumbariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru nanimshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema ambaye ametujalia kuwepo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya hasa katika kuongeza fedha na kuongeza bajeti hii ili kufanya kazi. Amejitahidi vya kutosha kuhakikisha maafisa ugani ambao kwa muda mrefu walikuwa hawaonekani na hawana vitendea kazi wameletewa vifaa vya kufanyia kazi pikipiki; sasa kilichobaki ni kuhakikisha tunawasimamia hawa maafisa ugani ili wafanyekazi ili kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa kuendelea katika sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Bashe, ni kijana msikivu, mwenye kupenda hasa na ana imani kuwa anataka kuleta kilimo chenye maendeleo vilevile nimpongeze Mavunde, nimpongeze Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu Bwana Tumbo ambaye huyu ni mtaalamu wa masuala ya vifaa vya kilimo alikuwa CAMARTEC, amekuja pale, naye ni mchango mkubwa katika maendeleo ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumza kwa muda mchache sana kutokana na muda nilio nao, na nitakwenda kwenye dhima. Dhima ya kilimo ya kwanza ni kuandaa kilimo bora chenye mazingira bora, lakini vilevile kuwaandaa wakulima wapate tija katika kilimo hicho pamoja na kutengeneza mifumo ya kimasoko ambayo itawasaidia wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile muda nilio nao nitazungumzia Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma. Ni mikoa ambayo sasa hivi kama Serikali haisimamii itaonekana na mikoa ya kimasikini wakati ni mikoa tajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kunatakiwa kuwepo na mifumo ili mifumo hii iweze kuitoa hii mikoa. Itakuwa ni aibu ukienda mikoa mingine inaonekana iko busy inafanya kazi, kuna viwanda kuna maendeleo; lakini Mkoa wa Lindi na Mtwara hatuna viwanda, bandari hazifanyi kazi, njia kuu zote za uchumi zikiwemo barabara ni mbovu sasa unategemea watu hawa watafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninazungumzia kutokea Songea mpaka Bandari ya Mtwara ina- kilometa 657 lakini kutoka Songea kwenda Dar es Salaam ni kilomita 948 lakini kutokana na urasimu wa bandari ya Mtwara ambayo Serikali hajijataka kuwekeza mizigo yote na nafaka na mazao yanakwenda katika bandari ya Dar es Salaam. Jiulizeni, Bandari ya Dar es Salaam kuna nini ilhali ukiangalia Bandari ya Dar es Salaam sasa hivi iko busy kiasi ambacho watu wanakaa na mizigo zaidi ya wiki nzima na urasimu huu unafanya kuingia katika corruption katika bandari ya Dar es salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Waziri ashirikiane na Waziri wa Fedha na Waziri wa Ujenzi waje watupe taarifa kuna nini mpaka bandari ya Mtwara mapaka sasa hivi haifanyi kazi. Urasimu uliokuwepo katika bandari ya Mtwara mizigo yote inayotoka Lindi na Mtwara na Ruvuma inabidi iende Dar es Salaam, hivi jamani kweli tunapiga hesabu za kibiashara hapa? Inamaana hakuna biashara inayofanyika hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ufuta unalimwa Kilwa barabara ya Liwale hakuna lakini ufuta ule ule unabidi uzunguke mpaka Lindi, Lindi mpaka Dar es Salaam ilhali Bandari ya Mtwara iko karibu. Hiki ni kitu ambacho mimi sielewi; ni kama ni zig zag ambalo naliona kabisa. Mimi nitataka nitachangia tena katika Wizara ya Fedha, watuambie Bandari ya Mtwara na Tanga zimekwama wapi? Mazao yote yanakwenda Dar es Salaam, tumeifanya Bandari ya Mtwara ikose kazi kwa ajili ya kupeleka mizigo yote Dar es Salaam. Wao wanatoa sababu za wafanyabiashara, lakini mimi hiyo wala haingii akilini. Kama kweli kuna mikopo inaweza kusaidia Bandari ya Mtwara wakaleta makasha mimi naomba Serikali isimame na hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumzia biashara za korosho, Kawaha na biashara mbalimbali ambayo iko katika mikoa hiyo, kwa kweli inasikitisha, inasikitisha kwasababu hawajatengenezewa mazingira rafiki, viwanda vyote vimefungwa. Hapa Tanzania Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alitengeneza biashara kikanda na mazao kikanda. Mkoa wa Lindi ulikuwa ni mkoa wa kulima karanga, soya, ufuta, na kahawa; ndiyo ilikuwa mikoa hiyo. Lakini mikoa mingine ilikuwa imetengenezewa kama pamba, Mikoa ya Kanda ya Ziwa wanalima pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Mikoa ya Lindi sasa imetiwa umaskini kwa ajili ya mifumo mibovu ambayo haijataka kuwa rafiki wanawananchi wa Mikoa ya Lindi ikiwemo bandari na barabara, lakini vile vile mazao hayana soko, viwanda mmefunga unategemea watanda wapi? Leo unachukua korosho unaipeleka nje as raw material, korosho ile ile ukibangua mwenyewe unakuja kuuza Dodoma shilingi 25,000. Je, tutaondoaje umasikini kwa watu wa Mkoa wa Lindi na Mtwara tukiwa na mifumo mibovu ambayo haiku rafiki na haiongei?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia tena wakati wa Wizara ya Ujenzi watueleze kwanini Bandari za Mtwara na Tanga hazifanyi kazi? Tujue, kwanini Barabara ya kutoka Kilwa mpaka Liwale haifanyi kazi? Kila mpaka Nachingwea watu wanaangaika na mazao. Unategemea watu wale watategemea nini? wataendelea kuwa maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli naunga mkono lakini sifurahi, nataka nione kabisa mfumo wa kilimo katika mikoa hii ya Lindi inapewa kipaumbele ili wananchi wale wasionekana kama ni wananchi maskini. Hii ni mikoa Tajiri, hivyo inahitaji msukumo na mfumo ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru na nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma kwa kutujalia nan kutupatia afya njema tukawepo hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya kwa kuitangaza Tanzania katika kuongeza diplomasia ya Kimataifa na sasa hivi naona hali ya Tanzania kutambulika katika Umoja wa Mataifa na duniani inakuwa kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru Mheshimiwa Waziri Mama Mulamula, Balozi Mbarouk - Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu. Hii timu yote ilikuwa katika Balozi mbalimbali, kufanya kazi kwao hapa ina maana wamekuja kutuongezea uwezo na juhudi walizozipata, maarifa waliyoyapata ili kutuongezea na sisi kuweza kufanya kazi vizuri katika hii Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge ni mhimili kama mihimili mingine ambayo ni Mahakama na Serikali Kuu na sisi tunapenda watambue kama mhimili wa Bunge lazima utambulike katika masuala ya kimataifa. Kunafanyika mikutano mbalimbali na maazimio mbalimbali ya Umoja wa Mataifa, ya Commonwealth, kuna summit mbalimbali lakini bahati mbaya muda mrefu hatujapata mrejesho. Nitoe mfano katika Umoja wa Mataifa kuna maazimio kila mwaka yanapitiwa iwe maazimio ya usalama, maazimio ya haki za binadamu ikiwemo walemavu, haki za wanawake, haki za watoto, haki za vijana na maazimio mengine ya Umoja wa Mataifa kuhusu United Nations for Climate Change. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maazimio yale yote hayafiki Bungeni tukayafanyia kazi. Hivyo Wabunge wengi wanapata taarifa zao aidha wasome katika mitandao, lakini je, utaitegemea mitandao wakati saa nyingine katika mitandao kuna taarifa ambazo sio za kawaida, ni fake news. Hivyo tunaamini kabisa wao kukaa kule walete yale maazimio yaliyotoka kule ili yaje katika mhimili wa Bunge, katika kuleta katika mhimili wa Bunge, Bunge itaifanyia kazi na ikiifanyia kazi sheria ile itakuwa inawasaidia kwenda chini. (Makofi)

Mheshiiwa Naibu Spika, nataka ni-declare interest mimi ni mlemavu, lakini ulemavu wangu sio wa kuzaliwa ni wa kupata ajali ya gari. Tuna maazimio yanapita kila mwaka katika Umoja wa Mataifa, lakini kutokana na Bunge halipati taarifa za watu wenye ulemavu tunapata taabu sana ushiriki wetu katika mikutano ya Umoja wa Mataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano leo ukitaka kwenda kuhudhuria mkutano ule wanaleta mlolongo lazima upitie Wizara ya Sera, Kazi, Ajira na kama Waziri haendi basi ina maana watu wengine hata taasisi zingine iwe SHIVYAWATA, CHAWATA watu ambao inabidi nao wakashiriki katika Mikutano ile jibu wanakuambia kwa vile Waziri haendi na ninyi wengine mnakosa fursa, hii kitu lazima muirekebishe.

Nishukuru jana nilikutana na Naibu Katibu Mkuu kwa kweli inabidi nimpongeze Mama Fatma nafikiri ni mama ambaye ana uelewa mkubwa na kutokana na uzoefu aliokuwa nao, amenifariji sana na amefanya kazi ya ziada kuhakiksiha haki za watu wenye ulemavu zinafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndani ya Umoja wa Mataifa ndio sisi ni wanachama Tanzania ni mwanachama wa Umoja wa Mataifa na kama ni mwanachama wa Umoja wa Mataifa, sheria na maazimio yale yakifika huku kwetu yanateremka mpaka chini kwa ajili ya kufanyia kazi na kujua haki zao ni nini. Lakini matokeo yake hivi vitu vinapuuziwa huu ni mwaka wa tano Tanzania hatujashiriki katika Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Watu Wenye Ulemavu. Matokeo yake kama wao hawaendi na huku chini kote watu wanashindwa kufanya kazi. Vyama vya watu wenye ulemavu havihudhurii kwa ajili ya urasimu ambao umewekwa na nataka nitambue tena, Bunge ni mhimili, hatutaki tena mpitie milolongo mingine pelekeni direct katika Bunge, Spika apokee taarifa zetu na azifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hivyo itakuwa tunapata taabu, ndani ya Bunge kuna Kamati hizi Kamati inabidi zitumike kwa kupitia mhimili wa Bunge. Kwa mfano, kunapita Mikutano ya Umoja wa Mataifa kutokana na Mabadiliko ya Tabianchi (United Nations for Climate Change), lakini Wabunge hawahudhurii wala Kamati haijui chochote, sasa matokeo yake unajiuliza sisi tumekaa hapa kufanya kazi gani, tunakuja hapa kufanya kazi na wenzetu duniani wanafanya nini. Mwaka 2007 tumekwenda kuridhia haki za wenye ulemavu katika Umoja wa Mataifa Watanzania tulikuwa watano, Kenya alikuja mtu mmoja lakini nimekwenda tena mwaka 2016 Wakenya wako 80. Hivi vitu msivione kama ni vya kawaida vinaturudisha nyuma kiupeo wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapohudhuria Mkutano ule sio unahudhuria kwa ajili ya walemavu kuna masuala ya uchumi, kuna masuala ya ajira, kuna masuala ya elimu, kuna masuala mbalimbali ya maendeleo ambayo sisi tunayakosa tuko katika kisiwa ambacho kinabidi kisiwa hiki kiongezwe kiweze kufanya kazi ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mabalozi nimelizungumzia karibu mara mbili kila Balozi ajitathmini katika Balozi zake je, niko hapa kwa kufanya kazi gani? Kazi ya kwanza ya Balozi kuiangalia Tanzania inanufaika vipi na kilimo, inanufaika vipi na uchumi wake na kuitangaza pale na pawepo na ma-desk maalum ya kuitangaza. Nilikuwa nazungumza mimi nakwenda pale New York lakini unakuta desk la utalii halina kazi maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mama ameipeleka royal tour duniani je, kama ma-desk haya hayafanyi kazi hizi royal tour hazitakuwa-sustainable kabisa, hatutaweza kufanya kazi. Ni lazima wajitambue kama wako pale kuisimamia nchi ya Tanzania iweze kuondokana na umaskini twende katika uchumi na uchumi ni ku-share resource baina ya wenzetu na sisi. Kama watakaa pale hawajitathmini basi haina haja ya kuwapeleka watu ambao hawana nafasi katika Balozi zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia suala la mjusi narudia tena. Mjusi Dinosaur ni haki ambalo lipo Ujerumani sitaliacha hili mpaka ufafanuzi upatikane, ule ni uchumi na kama uchumi ule wa Dinosaur ambaye yuko Ujerumani Lindi hatufaidiki na chochote. Si hivyo tu mwanzo nikafikiri ni nchi kumbe ni kikundi/taasisi kimechukua lile Dinosaur wanafanya biashara, wanafanya uchumi mkubwa kuhusu Dinosaur lile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jiulize mapato yanayopatikana ndani ya Serikali ni yapi; tuna royalty gani ndani ya Serikali ni yapi; je, Balozi wetu ambaye yupo Ujerumani anatuambia nini anatupa ripoti gani kuhusu mafanikio ya mjusi wanayoyapata wale vs nchi yangu, mkoa wangu na Lindi yetu nayo ifaidike na mjusi. Haiwezekani, maana yake sasa hivi taarifa tulizokuwa nazo mijusi yote mikubwa sita au Dinosaur makubwa sita yanatoka mkoa wa Lindi, ndege wakubwa 13 wanatoka Mkoa wa Lindi, lakini mpaka sasa hivi pamekaa kimya hakuna ripoti hakuna nini tunapeana tu kila mmoja anajiona mimi kama ni Wizara… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante, ahsante.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, Maliasili haina miliki ya peke yake ni Wizara ya Elimu na Wizara zingine na Wabunge vilevile tuna haki ya kupambana na mjusi na haki zetu zifanikiwe. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo naunga mkono, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. RIZIKI S. LULIDA. Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru sana na nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyetujalia kuwa na afya njema na kuwepo hapa. Ninamshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuitangaza Tanzania duniani na Royal Tour imetua ndani ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru Waziri, Mheshimiwa Mchengerwa, na Naibu wake Mheshimiwa Pauline Gekul kwa kazi kubwa wanayoifanya, Katibu Mkuu Ndugu Hassan Abbas na Naibu wake Ndugu Saidi Yakubu Majembe, vilevile niwashukuru BMT ikiongozwa na Ndugu Singo, anajua kabisa humu ndani anae Mama yake anaitwa Double Riziki, yeye ni Single mimi ni Double. Ninamshukuru Ndugu Neema Msita nae vilevile yuko BMT anafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie kuwa hii Wizara ni Wizara nyeti ambayo ikiwekeza vizuri italeta ajira kubwa sana kwa vijana. Ninaipongeza timu yangu ya Tembo Warriors, hii timu ni ya vijana shupavu, wenye ulemavu, ambao walipambana mpaka sasa hivi na wamesaidiwa na Serikali katika uwekezaji wao mpaka sasa hivi Tembo Warriors wanakwenda katika World Cup. Ninamshukuru Waziri Mkuu, Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa, akishirikiana na Mheshimiwa Rais walikuja kuwachangia uwanjani Shilingi Milioni 150. Ilileta chachu na hamasa kubwa kwa hawa vijana na ushindi wao sasa hivi tunaona unawapeleka katika World Cup. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawapongeza Serengeti Girls. Haya yote ni makundi maalum, mkiyaacha makundi maalum mngefanya makosa makubwa sana, kumbe makundi maalum yana uwezo mkubwa sana katika michezo. Leo nchi inapata faraja, inapata heshima kwa ajili ya makundi maalum ya walemavu na wanawake. Tujiulize, wanaume wako wapi, mimi naweka question mark, mtajitambua wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, klabu zote sasa hivi Tanzania ziwashirikishe makundi maalum ikiwemo klabu kubwa kama Simba Sports Club, nasema tena, kama Simba Sports Club. Wawe na kundi maalum la walemavu na wanawake, na timu kama ile ya Yanga Sports Club, nao vilevile wawaweke wanawake na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli ninaposema ni ajira nataka niseme ni ajira kweli. Tembo Warriors sasa hivi nina vijana wanne wamepata u-professional player, wameajiriwa huko Uturuki. Tayari tumefanya wapate ajira na wajitegemee wenyewe, ninataka kuwataja kwa majina na tuwapongeze. Ndugu Khalfani Kihanga, ni kijana mlemavu kutoka Tabora lakini sasa hivi yuko Uturuki. Ndugu Ramadhani Chomelo, huyu kijana anatoka Kisarawe sasa hivi ni mchezaji Uturuki. Ndugu Frank Ngairo, anatoka Iringa, sasa hivi ni mchezaji Uturuki, Ndugu Shadrack Hebron kutoka Mbeya. Jamani kazi ya vijana ni kubwa sana kuwasaidia hawa, tukiwekeza zaidi hapa ina maana tutawatoa vijana wengi watakwenda katika professional soccer, watakuwa wanajitegemea wenyewe, hawategemei tena kusaidiwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilichukuliwa watu wenye ulemavu ni watu wa kusaidiwa, Hapana! Watu wenye ulemavu wanajiweza wenyewe. Twendeni pamoja tuka-invest kwa watu wenye ulemavu ili waweze kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu sanaa; kwanza niwapongeze wasanii, katika sanaa vijana wameonesha kazi kubwa sana, sasa hivi wanaitangaza Tanzania duniani katika Royal Tour. Maana yake katika kutangaza utalii, unatangaza katika maeneo mbalimbali, utalii katika utamaduni, michezo, mila na culture mbalimbali yote yanaingia katika Royal Tour na Royal Tour nyumbani kwake ndiyo hapa michezo na utamaduni.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niwataje vijana ambao sasa hivi unaona wanawika na kuitangaza Tanzania duniani. Namba moja ni Diamond Platinumz; Harmonize (Konde Boy); Ali Kiba, Zuchu, Ray Vanny na wasanii wengine ambao wanaendelea kuonesha nchi katika maendeleo makubwa. Hawa watoto wanaonesha usanii na wameajiri watu na kuajiri watu ina maana na wao wenyewe wanajitegemea katika kuipatia mapato makubwa nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, matumaini yangu ni kuwa tusimamame na hawa watu na haya makundi ili tuweze kuitengeneza Tanzania yenye kujitegemea kwa kupitia usanii pamoja na michezo inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Royal Tour; mimi nakwenda kuitangaza nikiwa mmoja kati ya mabalozi wa utalii. Katika mabalozi wa utalii tunataka kuunganisha michezo na utaliii. Maana yake ni nini? Tunataka kuanzisha ndani ya mbuga zetu za wanyama waje wacheze mpira ndani ya Serengeti. Maana yangu ni kuwa ndani ya Serengeti na Ngorongoro kuna viwanja vya mpira, tukalete timu kubwa ziingie pale. Zitakapoingia pale baadae tutakuwa tunajiuza wenyewe na soko letu liko pale, kuwa leo timu ya Arsenal wanashindana na Manchester ndani ya Serengeti. Hapo tutakuwa tumemuunga mkono na hii itakuwa na shughuli ambayo ni very sustainable na itatuingizia mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapato yale tutakubaliana kabisa, fungu maalum litakwenda kwa ajili ya makundi maalum ili baadaye wasihangaike na mambo ya kutafuta chakula, mavazi, hata nguo za kuvaa iwe ishu, kuombaomba. Hakuna kuombaomba, wenyewe hawa wanajiweza, tukiwatengenezea mfumo mzuri watakuwa wanaweza kujipatia mapato yao bila kutegemea kuombaomba na sehemu nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina mengi sana ya kuongea, kwa siku ya leo ninaomba na kuwaunga mkono kwa asilimia kubwa sana kuwasimamia hawa vijana. Vijana wanakwenda katika mapambano makubwa ya World Cup na tusibweteke sasa hivi ndiyo kipindi cha kusimama nao. Nashukuru Tembo Warriors wanaondoka kwenda Poland, wamepata nafasi maalum kwenda kujiimarisha kwa muda wa siku kumi. Ninaomba tufanye kila njia tuwasaidie hawa watoto katika kwenda kwao huko wasipate taabu ya chakula au ya matumizi, na Wabunge tuna jambo letu, tunasema hapa tunanyamaza lakini Wabunge kwa pamoja tumeungana kuwapenda watu wenye ulemavu na wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeze vilevile Mheshimiwa Keisha, amekuwa ni mentor wangu, nae ameanzisha timu ya watu wenye ualbino nao wanakwenda Kenya. Kutokana na mfumo huu, tukienda katika mazingira hayo Tanzania yenye maendeleo ya michezo na utalii na kuingiza kipato katika sanaa ya vijana inawezekana. Nawashukuru sana na ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Upatikanaji wa Habari wa Mwaka 2016
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na mimi leo kuchangia katika hoja iliyowekwa mezani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna barabara isiyokuwa na kona, hivyo hata katika masuala ya siasa kona hazikosekani, lakini Mwenyezi Mungu mwisho wake atairekebisha na hali itakuwa nzuri. Nikitakie kheri Chama changu cha Wananchi (CUF) kitakwenda vizuri na Mwenyezi Mungu atatujalia kufika salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nami nichangie katika hoja iliyokuwa mezani. Kwa muda mrefu tulikuwa tunautaka huu Muswada ufike ili uweze kutusaidia na hasa katika maslahi ya nchi yetu ya Tanzania. Nataka nitoe mfano wa kwanza ambao mimi kwangu umekuwa ni mashaka makubwa, mfano ni TBC! TBCni Shirika la Utangazaji la Taifa, lakini kutokana na mazingira magumu ambayo yamekwazika katika TBC, leo ukienda Lindi na Mtwara hatuwezi kusikia TBC mpaka tunafika Vikindu. Hii yote kutokana na muda mrefu vilio vya Wabunge vya kutaka kusikilizwa na kupata taarifa, haikupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, TBC iliingia mkataba na Star Media, mkataba huu ulikuwa usaidie kusambaza na kupata taarifa mbalimbali za habari Tanzania nzima, jambo la kushangaza hawa Star Media wameingia mkataba na Star Times bila kuishirikisha TBC. Wameingia mkataba na Star Communication bila kuishirikisha TBC. Hawa TBC hawana meno hata hawaombi taarifa kwa nini kumeingia mikataba ya hivyo, waweze kujua mapato yanayopatikana, taarifa hizo TBC hawana!
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalizungumzia Shirika ambalo sasa hivi linakufa kwa sababu taratibu nyingi ambazo hazikufuatwa na wao wenyewe wanakiri kuwa hata wakiwaomba hawa Star Media waliingiaje mkataba mkubwa na Star Times ili angalau na wao waweze kujijua kimeingiwa nini, hapa kuna sintofahamu. Sasa tujiulize kama Wabunge kwa muda mrefu walikuwa wanataka kujua vinavyoendelea, leo tunaikuta TBC inakufa wakati imeingia katika uwekezaji mkubwa na Star Media. Napenda nipate majibu ni nini kinatokea TBC hajui kinachoendelea ndani ya Star Times.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wameingia katika suala la kuleta ving‟amuzi – Tanzania nzima tumepelekwa katika ving‟amuzi, wanasema wameendesha kwa hasara! Ningetaka kujua kwa nini wanawafanya wenzao wawe na mikataba ambayo haiwashirikishi na hata taarifa hawazijui, hii ni hatari kwa usalama wa nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja Tanzania Airport Authority, hili ni Shirika la Ndege linalosimamia viwanja vya ndege, nao wamekuja pale hawajui kinachoendelea! Tanzania tuna viwanja 600 katika viwanja 600, viwanja 58 tu ambavyo wao wanakuwa na authority navyo, matokeo yake hata wakiomba taarifa kwa viwanja vilivyobakia angalau usalama wa nchi uweze kujua, revenue collection zijulikane, mapato ya landing yajulikane, ni sintofahamu. Je tujiulize, kwa nini tumekaa kwa muda mrefu tukiacha vitu hivi vikiingia katika kikwazo kikubwa na kuifanya nchi iingie katika uchumi uliodorora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo Airport ambazo zipo tunaona kabisa unasikia Kenya leo wanauza Tanzanite, ndiyo wanarusha vitu kama hivyo. Tunaona leo kuna Airport ndani ya mbuga za Selous, ndiyo wanatoa pembe na wanaokota pembe katika maeneo hayo! Kutokana na taratibu hazikuwekwa za kupata taarifa hata katika Kamati za Bunge ukiomba ilikuwa hupati. Hii ni hatari katika nchi ambayo tunataka kwenda katika uchumi endelevu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja katika Halmashauri. Wabunge wote wanafahamu kama ni Madiwani, lakini baadhi ya Wakurugenzi hawataki kutoa taarifa za miradi mbalimbali matokeo yake unakuta shule zimeharibika, madarasa yako chini ya viwango, ukienda katika upande wa afya, hospitali hazina madawa, hela zinapelekwa lakini unapoomba taarifa inakuwa ngumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano katika kijiji cha kinyope, kile kijiji kimekaa kwa muda wa miaka 50 hawana hospitali, tukatafuta njia ya kusaidia na misaada mbalimbali tukapeleka pale mpaka leo nyumba ya Daktari haijajengwa. Watu wanahangaika kwenda sehemu mbalimbali kwa ajili ya kwenda kupata matibabu. Wanawake wanahangaika kutafuta kujifungua lakini sintofahamu! Ukiuliza au wanakijiji wakisema tunataka kujua kwa nini, anakuja DC anasema mimi ndiyo Rais wa Wilaya hii, umeleta maneno ya uchochezi na uwongo nakutia ndani. Sasa je, kama DC anawatisha wananchi kwa kutafuta haki zao na utaratibu wa habari, yeye anasema mimi ndiyo Rais, nchi hii itakuwa na Marais wangapi? Lazima sheria iseme, haya mambo ya kila DC Rais, basi hata mimi nitakuwa Rais ndani ya Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike mahali tusimamie haki, hawa watu wanaojenga kiburi kuwa mimi ndiyo Rais hawafanyi haki kwa wananchi, akiomba mtu taarifa basi taarifa hiyo atakayepeleka anatiwa ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaona misitu inakwisha, wanyamapori wanakwisha, lakini mwananchi atakayekuwa na taarifa akipeleka Polisi basi yule mwananchi wanamtia ndani! Tufike mahali Serikali isimamie sheria hii kwa makini maana inaweza kuja sheria lakini isisimamiwe. Watu wamesimama na corruption.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshukuru sana hii hoja imeletwa. Sasa ushauri wangu sheria hii hata kama imekuja kama hakuna usimamizi, basi itakuwa hakuna chochote ambacho kimeletwa hapa, tunaomba makucha yafanye kazi. Ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2017.
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninakushukuru kwa kunipatia nafasi hii, nimshukuru pia Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia nami kupata nafasi ya kuchangia katika hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya kwanza itaanzia katika uwindaji kutoa VAT kwenye leseni za uwindaji. Nataka ku-declare interest ni Mwenyekiti wa kupambana na ujangili ndani ya Bunge, lakini kuondoa tozo ya leseni ya uwindaji kwangu mimi inanikwaza vibaya sana. Tunaangalia mbuga ya Selous sasa hivi hamna wanyama; wale big five tembo, simba, nyati, faru, chui wote wametoweka kwa asilimia zaidi ya 70.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri hawa wawindaji wanaokuja wengi ni Professional Hunters ambao ni matajiri wakubwa sana, maana yake ni kuwa mnachangia wanyamapori kumalizika na kukandamiza uchumi wa utalii ambao unachangia asilimia 17.2.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa sababu za msingi kwa nini nasema hii tozo irudishwe watozwe kama watu wengine. TANAPA wanatoa tozo kwa Serikali billioni 33, lakini hawa wawindaji wanatolewa tozo, TANAPA akijenga barabara analipa kodi, akipeleka maji katika maeneo mbalimbali mbugani analipa kodi. Leo tunashangaa hawa wawindaji ambao wanamaliza wanyama, uchumi wa nchi utatoweka, wanaambiwa wasitoe tozo ya leseni ya uwindaji. Kwa kweli hatujawa serious kama kweli nchi hii tunataka kuingiza uchumi bora katika suala la sekta ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimezungumzia suala la mjusi muda mrefu lakini naona kama Serikali haiko serious, tunakimbizana na Mama Lishe, Ujerumani peke yake inapata Euro milioni 600 kwa mwaka, lakini hata mrabaha wa kupeleka pale anapotoka mjusi Tendeguru hatupati, bado tunaona pana silence, mnakimbizana na wanaouza mboga za majani, na nini, vitu ambayo unaona kabisa haviko sensible kabisa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaingia katika suala la uwekezaji, wawekezaji wa ndani tunasema tunataka tuwahamasishe, mimi pia ni Mwenyekiti wa kupambana na Malaria Tanzania, Tanzania without malaria is possible, lakini nishukuru Patron na Mwenyekiti wa Malaria ni Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete. Wao walipigania kuhakikisha panawekwa viwanda vya kutengeneza vyandarua ambavyo vina-quality ambavyo vitawasaidia Watanzania kuweza kupambana na malaria, jambo la kushangaza tumejaribu kupigania humu ndani hakuna uwezekano.

Mheshimiwa Naibu Spika, A-Z ni Shirika ambalo linafadhiliwa na Global Fund pamoja na USAID walituita kwa ajili ya mkutano na humu ndani wemefanya semina, wanatoa tax ya bilioni 17.7, lakini utashangaa wanaleta vyandarua feki kutoka nje ya nchi, hasa kutoka China, vyandarua vile havina viwango, havina ubora, je, huyu atafanyaje kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika purchasing principals ziko nne, you have to buy the right quantity, with the right quality, with the right price, with the right time. Leo unapoleta vyandarua vibovu kutoka nje mnafanya nini, je, mko tayari katika uwekezaji au mnataka kutubabaisha? Naomba majibu ya haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, hawa wanaleta ajira wanaajiri Watanzania wananchi hasa akinamama 8,000, leo wanafunga kiwanda kile, nani atapata ajira pale Arusha? Hii ni hatari kwa Watanzania, uchumi wa nchi utaangamia kwa ajili ya kuangalia viji-ten percent, siwezi nikasema kama ni hivyo, lakini kwa nini Waziri anababaika kuzuia tozo kwa hawa wa nje wawe zero wa ndani wanalipa kodi hii haiingii akilini kabisa. Tufike mahali tujitambue, hawa washauri wanaoishauri Wizara wanafanya kazi gani kitaaluma kusaidia vitu kama hivyo ambavyo vinaleta kigugumizi katika uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie masuala ya uwekezaji hasa viwanda vya ndani ambavyo vinatengeneza maji, juice, tunaingiza maji kutoka nje kwa asilimia 61, hawa ndani tozo yake ni shilingi 58, jiulize asilimia tatu hii ni kiwango kidogo, je watakuwa tayari ku-compete na wale wa nje?

Hawa wa ndani wanafanyakazi, wana ajira, wamewekeza, mnaruhusu maji na sasa hivi tunaona tuna bidhaa feki hata maji, vyakula kutoka nje, michele, mafuta ya kula, lakini bado tunapiga kigugumizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii iko katika dilemma, tunauza ufuta, nje tunapeleka ufuta nje, tunapeleka mbegu za pamba nje, tunapeleka mbegu za karanga nje, mbegu za alizeti nje, tunaletewa mafuta mabovu, nani wa kulaumiwa ni Watendaji. Inafika mahali unajiuliza mafuta yanatoka nje tayari yameshaganda ni mafuta ya nini, ina maana ni mchanganyiko wa vitu vichafu wametuletea Tanzania, lakini wanasema tunaingiza mafuta, hivi ina maana kila kitu lazima uingize. Kuna vitu vingine havihitaji kuletwa Tanzania, tuna viwanda vimefungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi kuna kiwanda cha Ilulu kilikuwa kinatengeneza mafuta ya ufuta na karanga mmefunga. Kulikuwa na viwanda vya pamba mmefunga, matokeo yake mnaagiza mafuta kutoka nje, kwa afya ya Mtanzania au mnataka kutuongezea magonjwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inasikitisha, ningeomba hili eneo mfute kabisa kuleta mafuta kutoka nje ni hatari kwa maisha ya Watanzania inatuangamiza, kuleta maji kutoka nje vilevile inatuangamiza. Kama wao wanataka kuja Tanzania watumie product za Tanzania ambazo zimekaguliwa ziko katika viwango, kutuletea vitu vichafu kwetu ni hasara na inatuumiza na ndiyo maana sasa hivi cancer ziko juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la maendeleo, miradi ya maendeleo Mkoa wa Lindi na Mtwara tuko nyuma. Miradi ya barabara Lindi na Mtwara ambapo korosho imeingizia pato la Taifa kwa asilimia kubwa sana ambayo haijapatikana katika mazao mengine yoyote, hakuna barabara ya kwenda Liwale, hakuna barabara ya kwenda Nachingwea, hakuna barabara ya kwenda Milola.

Je, tutafikaje katika uchumi bora ikiwa sisi kila siku tunapeleka uchumi bora wa mazao lakini tumewekwa nyuma Mkoa wa Lindi na Mtwara tuko nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nisikatae bajeti hii kuwa haiwatendei haki watu wa Kusini, hivyo silazimiki na wala siwajibiki kusema ndiyo wakati naona kabisa kuwa Mikoa ya Lindi na Mtwara kusema ndiyo kwa wachache ambao watanufaika, lakini kwa mimi nasema hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya wa Mwaka 2017
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru vilevile kwa kunipatia nafasi hii. Mimi ni mdau na mkereketwa wa kuwasaidia vijana ambao wanatumia dawa za kulevya. Na nitakuwa mkweli daima kuwapongeza wale wote ambao wako kipaumbele kusimamia suala la dawa za kulevya. Yeyote ambaye hajaathirika katika familia yake hatakiwi kubeza kwa vile katika nyumba nyingi akina mama wengi wanasumbuliwa na vijana wo katika suala la dawa za kulevya; hivyo nitawapongeza wote waliokuwa katika ukereketwaji huu, iwe Mkuu wa Mkoa, awe nani, mimi kwangu namfagilia kwa big up, kuwa aendelee kusimamia kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea tena kuhusu airport. Walikuja Wakurugenzi wa TAA (Tanzania Airport Authority), Tanzania tuna airport 58, lakini tisa tu ndizo zilizo chini ya Serikali zilizobakia zote ni njia za panya, kinachofanyika kule ndani hakijulikani. Sasa jiulize kama tuna airport 49 mimi na wewe hatujui kinafanyika nini na airport nyingine ziko ndani ya visiwa vidogo vidogo kama Kisiwa cha Tanzhovu, Kilwa. Sasa unajiuliza sehemu kama hizi Serikali hata Mbunge hata mtu yeyote haruhusiwi kwenda pale, ni mianya ambayo ni hatari kwa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na utaangalia wazi kuwa maeneo ambayo yameathirika ni kandokando ya bahari kuanzia Mtwara mpaka Lamu. Mombasa sasa hivi imeshakufa hata hoteli zote zimefungwa kwa ajili ya biashara ya dawa za kulevya imekuwa kubwa, hivyo Zanzibar, Dar es Salaam pamoja na Tanga nao wamekuwa waathirika wakubwa wa dawa za kulevya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie sana hasa njia panya za baharini katika mikoa hii. Watu wanatumia majahazi kuingiza dawa za kulevya kwa kupitia bandari bubu. Watu wanapitia katika mitumbwi kuleta dawa za kulevya kuingiza nchini, tusimamie hilo, ni eneo ambalo watu wanatumia nafasi hiyo kuiangamiza nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni shahidi, airport ya Dar es Salaam VIP wanakuja watu wengi ambao sio VIP; wanakuja watu unashangaa delegation ina watu 50 mpaka
60. Je, tunakagua wale watu kuwa wote ni VIP? Na mizigo yao mingi inakuwa haikaguliwi na kama haikaguliwi wanafanya nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, ni maeneo ambayo ni ya kuangalia. Sisi tunakwenda nchi za nje hatuthaminiwi kama VIP, lakini anakuja mtu mchovu tu ameipata alikoipata huko passport yake anakuja pale anathaminiwa na anapita pale na mizigo yake bila kukaguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikupe ufafanuzi kuhusu suala la uplift ya Dar es Salaam Airport. Unaingia ndani ya uplift, mgonjwa mmoja ana watu wanne wote wamembebea mizigo, unajiuliza mizigo hii ya nini? Mizigo inapita katika nia ya kawaida. Halafu unafika pale chini unaambiwa lift haifanyi kazi, anapitishwa katika njia ya kawaida, anachukuliwa na magari kama ambulance na kila kitu anaondoka na mizigo ile na watu wale wanaondoka katika maeneo kama hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba maeneo ya airport ya Dar es Salaam, hasa eneo la VIP likaguliwe kwa makini sana. Na wale wanaokuja na passport zao waangaliwe hivi ni kweli wale wote wamekuja na delegation ile ni watu ambao mizigo yao haikaguliwi? Ni mianya ya hatari, ni mianya ambayo inawafanya Watanzania na vijana wetu kuangamia katika suala la dawa za kulevya bila kuwa na msaada wowote.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakuja katika sober house. Vijana wanapelekwa pale wanapewa nafasi ya kuelimishwa, lakini baada ya pale anafanya nini? Hana kazi ya kutosha, hamjamtafutia shamba akalime, hamjamtafutia mazingira ambayo akitoka pale atafanya nini. Anakwenda kukaa mtaani akiwa hana kazi, hana shughuli ya kufanya, matokeo yake yule kijana atakuwa tayari anarudi tena kurudia yale yale, hapa tutakuwa bado hatujaifanyia mema sheria hii, ili iwasaidie hao vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sina mengi, nasema ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Serikali Mtandao wa Mwaka 2019
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru i kupata nafasi hii kuchangia hoja ambayo iko mezani. Kwanza ninaunga mkono hoja hii kwa asilimia 100 kwa vile kwangu naona italeta mafanikio makubwa na kuboresha uchumi wa nchi ambao utakuwa katika mahali ambapo salama kama takwimu zetu tunazoziandaa zitakuwa katika usalama zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi uchumi ukitaka uwe sahihi ni lazima uwe na data ambazo ziko protected. Maana yangu ni katika data kuwa protected lazima kutakuwa na usalama wa hizi data tulizokuwa nazo. Kwa mfano nilipongeze Shirika la TANESCO hata kama bado kuna mapungufu lakini leo nikitaka kununua LUKU sipati taabu, ninaingia online, nalipia na kupitia katika Taasisi zote hizo, baadaye nalipia luku yangu napata umeme najikuta nakwenda vizuri sana. Maana yake ni unakuwa na imani unachokituma na ulichokipata unakiona na wao wenyewe kule katika data zao wanaziona na hata Serikali ikitaka kufuatilia data zile inakuwa ni rahisi kwa ajili ya kuthibitisha nini kimefanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakuja mashirika mengi yanataka kuingia katika mfumo huu wa mtandao lakini nataka kuweko na mabadiliko katika mfumo hii ili tusilete changamoto ambazo zingine hazina mfano. Nitoe mfano, nimeipongeza TANESCO inakuja DUWASA/DAWASCO wanabadilisha control system kila mwezi unapolipa maji nikilipa maji leo mwezi huu napewa code number nyingine na control number nyingine, nikiingia mwezi ujao, control number nyingine, namba nyingine na mtumiaji mwingine kwa majina mengine. Maeneo kama haya ni mianya mikubwa ya upotevu mapato ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata taarifa juzi DAWASCO inakwenda zero, wanakwenda zero wakati kama wana mifumo kama hii ambayo ilikuwa imepangiliwa vizuri isingekuwa na urasimu wa kujikuta wanakwenda biashara zero, unalipa bill, bill nyingine inakuambia NMB imepokea pesa halali za Mheshimiwa Riziki Saidi Lulida 30,000. Muda mwingine unalipa unaona kimya hakuna kinachoendelea, mifumo kama hivi kama haikusimamiwa hata hizo data utakazopewa itakuwa za kupikwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini cha kufanya? Baadhi ya mashirika wawe na system ambayo inafanana isilete usumbufu. Kwa mfano leo sitaweza kukaa Lindi wakati niko Dodoma, nataka kulipa Lindi wananiambia tayari wameshanibadilishia control unit yangu mpaka kuipata ya Lindi itanichukua miezi miwili, tayari nimepata usumbufu mkubwa. Lakini kama inavyokuwa lwo LUKU, sipati tabu kabisa, hivyo DAWASCO wajiulize, wajitathmini ili waufanye mfumo wao usiwasumbue wananchi au wateja wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, data protection inakwenda sambamba na data communication, data communication tutazipata wapi? Kwa kupitia mitandao ya TEHAMA kama TIGO, Airtel, Vodacom na mingine, kuna SASTEL na mingine. Je, maeneo yale tumeingia nao ubia, sisi tuko wapi? Walikuja watu wa Airtel kutoka namba moja mpaka system nzima inakuwa inamilikiwa na wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika hizi hela zetu tunazopitia katika hiyo mifumo mnazisimamiaje? Kunakuwa na mapungufu makubwa, husimamii! Eneo la data protection ni la usalama. Je, tumewaandaa vijana kukaa katika maeneo hayo wenye kuwa na uwezo kusimamia vitu kama hivyo, sio kutaka kusema kila mmoja anayekwenda kukaa pale lazima akawe pale, lazima iwachuje, iwafanyie vetting nani viongozi katika idara hiyo. Pale utaona usimamizi unakuwa bora. Lakini ukimuweka yeyote akakae pale kwa kuwa anaijua ICT, IT ndiyo maeneo ambapo panaingia uchakachuaji. Unachakachuliwa kwa kupitia hackers au watu wakaingiza viruses tu basi, mara moja nchi ikaingia katika dhahama kubwa, pesa ya kwenda katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mawasiliano ya pili na kwa kupitia hiyo hiyo mitandao, leo unaenda kwa mfano kuna siku nilikwenda Ngorongoro siku nzima mtandao haufanyi kazi hivyo hela yako inakaa juu kwenye benki haifiki wala ilikotoka hairudi na mtumiaji anakuwa amekaa katikati hapa. Je, mazingira haya ya mawasiliano duni na sisi tunakwenda katika mtandao mkubwa wa digitaly na Wakala wa Mtandao wa Serikali hili mmeliwekaje? Maana yake kuwa watu wa mawasiliano na wa mitandao hii ya mawasiliano iende sambamba na Serikali, ama la! Wizi wa mitandaoni ndiyo unapitia hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajiona sisi wenyewe katika hela ndogo ndogo tu watu wanapigia milioni moja milioni mbili, je, katika mitandao mikubwa kama hivyo ni bilioni ngapi yanayoibwa kwa kupitia mitandao hiyo na collision inakuwa ya sisi wenyewe wafanyakazi kwa kutumia na hackers mbalimbali ambao wana collude katika biashara namna hivyo, ni kitu kizuri lakini kama hakina usimamizi ni hatari sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, uchumi mkubwa tunaoutegemea Tanzania sasa hivi ni kilimo na mazao makubwa ya kilimo kama pamba, kahawa, korosho tayari yana mtandao mkubwa kiuchumi. Nataka nirudie tena mwaka 2017/2018 tuliweza kupata trilioni 1.2 kwa vile zile hela ziliweza kusimamiwa je, maeneo kama hayo Serikali inaisimamiaje ili kutengeneza mitandao ambayo hela zile za wakulima hazitapata hasara iwe kwa mkulima au kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe mfano, mwaka jana watu wa vijijini waliambiwa kafungue akaunti katika benki, hela zao zote zitapitia katika benki. Usumbufu waliokutana nao wananchi ni mkubwa, anakwenda anapima koroshio zake, anaambiwa korosho zako za milioni 5, akienda benki CRDB jina lake halionekani, akienda NMB jina lake halionekani. Alichoandikiwa huku sicho kilichokuwa kule. Ndiyo hapo ninaposema je, hizi data protection kwa wananchi iwe mkulima, iwe mlaji, iwe mtumiaji, iwe mtu wa mwisho Serikali mmezisimamiaje? Ni hatari katika uchumi lakini kama nchi hii tutakuwa hakuna usimamizi mzuri itakuwa nchi hii tumekwenda vizuri na ni kitu ambacho ni kizuri na kitatusaidia katika masuala yote ya uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitawapongeza zaidi taasisi ambazo zimeweza kufanya mazuri na tujifunze kwao, mtanisamehe sana pengine itaonekana nataka kuleta upendeleo. Ngorongoro wameweza kuutumia mtandao huu kwa muda mrefu, uchumi unakua siku hadi siku kwa kuwa wanaweza kuboresha. TANAPA mabadiliko haya ya mtandao wao wametumia kwa muda mrefu na kwa kweli wao wametoka bilioni 50 mpaka bilioni 200, haya mashirika lazima tuseme ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Bandari wanakwenda vizuri lakini leo tunaona mashirika kama TANESCO wanakwenda zero, DAWASCO zero, DAWASA zero lakini maana yake ni, hawajaboresha. Ukienda Lindi, mtandao haufanyi kazi wa maji, wala wa TANESCO Lindi hamna, ukienda Mbeya unaambiwa DAWASCO unajitegemea kwa kutumia analog kuchanganya analog na digital maana yake tumejichanganya hata katika data collection zetu zitakuwa za kupikwa, na kama tunapata data za kupikwa, tusitegemee mabadiliko makubwa ambayo tunaweza kuyapata. Tuhakikishe Serikali inayasimamia haya mashirika ambayo yanakwenda vizuri taarifa zao na data zao zikae vizuri ili kuufanya uchumi huu wa nchi uweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)