Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Susanne Peter Maselle (6 total)

MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika,Serikali inatoa kauli gani kwa Jeshi la Polisi kupitia askari wasio waadilifu wanaokamata watu hasa viongozi na wafuasi wa UKAWA na kuwaweka mahabusu kwa zaidi ya saa 24 bila kuwapeleka mahakamani wakijua kwamba wanavunja sheria kwa kuwabambikizia kesi za uchochezi na CyberCrime? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi linapokamata watu huwa haliangalii itikadi zao na linapowafikisha watu mahakamani haliwaulizi kadi ya chama alichonacho, bali Jeshi la Polisi hukamata watu kufuatana na kosa alilofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kwa Watanzania wengine, akishakamatwa, kuna hatua ambazo zinafanyika na baada ya hapo anafikishwa mahakamani. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. SUSANNE P. MASELE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Ni lini sasa Serikali itaondoa hii dhana ambayo imeanza kujengeka kwamba Serikali haiwezi kuajiri kwa sababu haina fedha na kwamba Mheshimiwa Rais ndiye amekuwa akiajiri kwa utashi wake bila kufuata sheria?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali inajigamba kwamba imekusanya mapato mengi na imeondoa Wafanyakazi hewa, lakini ni kwa nini haijapandisha mshahara wala kupandisha watu madaraja? Serikali iwaambie Watumishi, ni kwanini haifanyi hivyo? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa napenda kusema hakuna dhana kwamba Serikali haina uwezo wa kuajri. Wote mnafahamu katika mwaka wa 2015/2016 mazoezi yaliyokuwa yakiendelea katika uhakiki, lengo letu kubwa lilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na idadi ya rasilimali watu ambayo tuna uhakika nayo, pia kujiriddhisha fedha ambayo tunalipa kama kweli ni thamani ya fedha kulingana na rasilimali ambayo ipo kazini.
Mheshimiwa Spika, tunashukuru kwa kufanya hivyo, tumeweza kuondoa zaidi ya watumishi hewa 19,708 ambao endapo wangeendelea kubaki katika orodha ya malipo ya mshahara, wangeisababishia Serikali hasara kila mwezi ya zaidi ya shilingi bilioni 19.8 fedha ambazo zingeweza kwenda kutumika katika miradi mingine ya maendeleo ya nchi.
Mheshimiwa Spika, ukiangalia tu katika mwaka huu wa fedha, tayari katika bajeti yetu tuliji-commit kama Serikali kwamba tutatoa ajira katika mwaka huu wa fedha 2017/ 2018 zaidi ya ajira 52,436. Pia tumeshaanza, ukiangalia katika mwaka huu wa fedha ambao tulikuwa tunaumalizia mpaka Julai, tayari tumeshatoa zaidi ya vibali vya ajira 10,184 na zaidi ya vibali vingine 4,816 pia viko katika taratibu za kutolewa kwa ajili ya kuziba mapengo yaliyojitokeza kutokana na suala zima la vyeti vya kughushi.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala zima la kupandisha mishahara pamoja na vyeo au madaraja; katika suala la mishahara, mwaka huu kilichofanyika na nimekuwa nikilisema mara nyingi, ni kweli hatujapandisha mishahara. Hatujapandisha mishahara kwa sababu bado tunaendelea kuangalia hali ilivyo, pia na hali ya kiuchumi.
Mheshimiwa Spika, tulichokifanya kwa mwaka huu ni nyongeza ya miashahara ya mwaka ambayo ni annual increment na wakati wowote kuanzia sasa nyongeza hiyo ya mishahara ya mwaka itaanza kutekelezwa.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa madaraja, tayari fedha ilishatengwa. Kuna zaidi ya shilingi bilioni 660 zimeongezeka katika bajeti ya mwaka huu ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2016 iliyokuwa shilingi trilioni 6.6. Mwaka huu tumetenga zaidi ya shilingi trilioni 7.205 na hii itasaidia kulipa maadeni ya watumishi, itasaidia pia kupandisha watumishi zaidi ya 193,166 na tunaamini wakati wowote stahiki hizo watumishi wataweza kuzipata.
Mheshimiwa Spika, hayo ndiyo maelezo ya Serikali na hakuna dhana iliyojengeka kwamba hatuwezi kuajiri wala kupandisha mishahara. (Makofi)
MHE. SUSANNE P. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, baada ya taratibu kukamilika, je, Serikali itachukua muda gani kuwapatia leseni wachimbaji hao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, yamejitokeza madai kuwa zuio la mchanga pale bandarini makinikia halikuwagusa wachimbaji wakubwa tu hata wadogo pia.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba wachimbaji hao wadogo wanasafisha mchanga wao hapa nchini ili kuendeleza uwekezaji na kutengeneza ajira zaidi kwa wachimbaji hawa wadogo? (Makofi). Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. DOTO M. BITEKO): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itachukua muda gani, naomba nimjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba, taratibu za kuunda Tume ambayo ndiyo imepewa mamlaka ya leseni ya uchimbaji madini, iko katika hatua za mwisho za kuundwa. Mara itakapokamilika kazi hiyo itaanza mara moja, kwa hiyo, haitachukua muda mrefu sana baada ya Tume hiyo kuwa imeshakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili la zuio la mchanga, naomba nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Watanzania, kwamba Sheria ya Madini haijazuia usafirishaji wa michanga nje ya nchi isipokuwa zipo taratibu na sheria ambazo yule mtu anayetaka kusafirisha mchanga kama madini lazima azifuate kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba tumezuia yale makontena kwa sababu yalikuwa na mgogoro ambao Serikali tuliona kuna haja ya kujiridhisha kabla ya kuruhusu.
Mheshimiwa Mwenyekti, kama kuna wananchi ambao wana madini ya mchanga ambao wanataka kuyasafirisha kwenda nje ya nchi kama wengine ambavyo wanapata vibali na wao wafuate taratibu watapewa vibali. (Makofi)
MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa nini operesheni za Serikali dhidi ya uvuvi haramu zimekuwa zikijikita katika kutekeza zana haramu za uvuvi badala ya kujikita katika kuwasaidia wavuvi hawa waweze kupata zana hizi halali kwa urahisi na kwa bei nafuu kwa kuwaondolea kodi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa uvuvi haramu unaelezwa kama moja ya tishio la kutoweka kwa samaki adimu kama ningu, nembe, gogogo, ngogwa, domodomo, sangara, njegele na sato katika Ziwa Victoria. Je, kuna mkakati wowote wa kusaidia samaki hawa kuzaliana tena ili kuendeleza fahari ya ziwa hilo na mazao yake?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini operesheni za Serikali zinajikita kuteketeza nyavu badala ya kuwapa nyavu halali? Operesheni za Serikali zinafanyika kwa mujibu wa sheria na operesheni hii inayofanyika kwa maana ya Operesheni Sangara inafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Uvuvi Na.22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwapa nyavu za bei nafuu wavuvi ni utaratibu ambao tunao pia na ndiyo maana tumetoa punguzo la kodi na hata kuondoa baadhi ya kodi katika vifaa hivi vya uvuvi ili kusudi kuweza kuwasaidia wavuvi wetu. Kama haitoshi tumeanzisha programu maalum ambazo kwa kutumia hata Mifuko yetu ya kijamii kama vile NSSF kuwafanya wavuvi waweze kujiunga katika vikundi ili waweze kupata mikopo na kuweza kununua nyavu kwa bei nafuu na vifaa vingine kwa ajili ya shughuli za uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, ni kutoweka kwa samaki kama vile gogogo, nembe na furu. Tumeendelea kufanya tafiti mbalimbali kwa kutumia taasisi yetu ya utafiti ya TAFIRI ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kulinda rasilimali hizi za nchi kwa ajili ya vizazi vya leo na vizazi vijavyo. Tunawaomba Waheshimiwa Wabunge wote waweze kutuunga mkono katika jambo hili kwa manufaa mapana ya Taifa letu.
MHE. SUSAN P. MASSELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu ya Serikali, ya Waziri, ambayo yanavunja moyo kabisa, kwa sababu hawajatoa commitment ni ni lini watamaliza huo ukarabati na ukizingatia Vyuo hivyo alivyovitaja viko kwenye hali mbaya sana na ukizingatia pia Jiji la Mwanza, ni Jiji ambalo linakua kila siku. Vyuo vingine viko uchochoroni kabisa ambapo ni mazingira mabaya kwa wanafunzi na Wakufunzi katika kufanya kazi. Sasa katika majibu haya nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, mwaka jana tuliona Serikali kupitia Tume ya Vyuo Vikuu Nchini (TCU) ikivichukulia hatua Vyuo Vikuu binafsi ambavyo havikuwa na vigezo vya Vyuo Vikuu na kuviacha Vyuo Vikuu vya Umma ambavyo vilevile vilikuwa havina vigezo vya kuwa Vyuo Vikuu kama alivyojibu kwenye swali la msingi. Je, Waziri haoni kwamba zoezi hili lilikuwa linagandamiza Vyuo Vikuu vya binafsi ambavyo vinatoa nafasi kubwa kwa wanafunzi ambao wamekosa nafasi kwenye Vyuo vya Umma na kupata nafasi?

MWENYEKITI: Sema tu straight.

MHE. SUSAN P. MASSELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Serikali ina ndoto ya Tanzania ya Viwanda ni lini sasa itajenga, Polytechnic College katika Mkoa wa Mwanza, ambapo itatoa ujuzi kwa ajili ya mahitaji ya viwanda ukiachilia mbali Chuo cha...

MWENYEKITI: Ahsante, inatosha. Mheshimiwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa niaba.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA K.n.y. WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Susanne Maselle, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, si kweli kwamba zoezi hili lililofanyika lilikuwa la ugandamizi na ndiyo maana vyuo ambavyo vilionekana vina matatizo havijalalamika, vimetii masharti, vimeboresha vyuo vyao na wale ambao wamekamilisha wamekabidhiwa kuendelea kufanya kazi. Kwa hiyo, hii siyo kweli lakini na vyuo vya umma pia vinazingatia utaratibu na ubora wa elimu kwa kadri ya miongozo iliyotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, tumesema nia ya Serikali si kuanzisha vyuo kila mkoa bali ni kuhakikisha vyuo vilivyopo vinaendelea kuboreshwa kwa kuongeza miundombinu na wataalam waliobebea katika nyanja hizo. Vikiimarishwa vinatosha kutoa wataalam kwenye viwanda na kubaki na kutumia utaalam wao nje ya nchi yetu.
MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Waziri amesema kwamba mradi wa kutoka Nyahiti umekamilika, siyo kweli, nilikuwa huko juzi. Mradi huo hautoi maji na Mkandarasi hayuko site na hili lilikuwa ni agizo la Mheshimiwa Rais kwamba miradi kama hii yote ikamilike na ifanye kazi. Sasa atuambie, Wizara imekaidi agizo la Mheshimiwa Rais? Je, ni lini wananchi wa Misungwi watapata maji ya uhakika ? Ukizingatia wako karibu kabisa na Ziwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Mwishoni mwa mwaka 2019 Serikali iliweka miundmbinu katika Kata ya Shibula na Bugogwa katika Jimbo la Ilemela, lakini maji hayatoki na yakitoka yanakuwa yanatoka kwa kusuasua na pia yanatoka machafu sana…

SPIKA: Mheshimiwa Susanne unahutubia badala ya kuuliza swali.

MHE. SUSANNE P. MASELLE: Mheshimiwa Spika, najenga hoja.

SPIKA: Aaah, uliza swali.

MHE. SUSANNE P. MASELE: Mheshimiwa Spika, ni lini sasa wananchi wa maeneo hayo watapata maji ya uhakika ili waweze kufaidi miradi hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, kwanza napenda kumfahamisha ndani ya wiki mbili nilikuwa katika Jimbo la Misungwi, nilikuwa na Mheshimiwa Mbunge na tumefanya kazi kubwa. Changamoto iliyokuwepo pale ilikuwa ni Mkurugenzi wetu wa Maji. Tumemwondoa na mradi huu mkubwa utasimamiwa na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira MWAWASA katika kuongeza utendaji. Mradi umekamilika kwa zaidi ya shilingi bilioni 12 katika kuhakikisha wananchi wa Misungwi wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la Ilemela pamoja na Nyamagana yake tuna mradi zaidi ya bilioni 38 tunatekeleza katika kuhakikisha wananchi wa Nyamagana pamoja na Ilemela wanapata huduma ya maji na nilikuwepo na Waheshimiwa Wabunge na wanafanya kubwa na nzuri na tumemwagiza Mkandarasi, kabla ya mwezi wa Tatu mradi uwe umekamilika na tutakwenda kuuzindua katika wiki ya maji. Kama tulivyosema, wiki ya maji haitokuwa wiki ya mapambio, wiki ya maji itakuwa ni kazi ya kuzindua miradi mbalimbali ya maji ikiwemo na Nyamagana. Ahsante sana. (Makofi)